Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Njalu Daudi Silanga (32 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naitwa Njalu Silanga, Mbunge wa Jimbo la Itilima, maarufu Mtemi unakotoka. Kwanza nianze kuwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Itilima kwa kuweza kuniamini kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga hoja ya Mheshimiwa Rais kwa hotuba nzuri aliyoizungumzia hasa inalenga vijana kupata ajira, amezungumzia suala la viwanda, nchi yetu imekuwa na viwanda vingi, viwanda vingine bado vinafanya kazi na vingine vilisha-expire.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Mheshimiwa Rais wasaidizi wake wakiifuatilia vizuri, na wakitekeleza kwa kasi wanayoifanya ni imani yangu tunaweza tukatoka hapa tulipo tukapiga hatua nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia viwanda ni lazima miundombinu yote iwe kamili, ninamshukuru Mheshimiwa Muhongo leo amejaribu kutoa ufafanuzi kuhusu mambo ya umeme. Viwanda vikubwa nchini lazima umeme uwepo saa zote, kwa sababu kiwanda kinapoendeshwa umeme ukikatika mwekezaji atakuwa na gharama kubwa sana.
Mheshimwa Mwenyekiti, jambo jingine ni lazima sasa Serikali ifike muda itenge maeneo maalum kwa ajili ya viwanda, na tunapozungumza viwanda maji yawepo na barabara ziwepo za kutosha hasa kule mali ghafi inakopatikana, utakuta maeneo mengi mali ghafi zipo lakini haziwezi kufika katika sehemu husika kwa sababu ya barabara hazipitiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kwenye Jimbo langu ninakotoka nashukuru sana Mheshimiwa Rais amempandisha Mheshimiwa Mbarawa kuwa Waziri wa Ujenzi, alipokuja kilometa kumi tulitumia saa mbili kufika tunakokwenda, kwa kweli ni hali tete na mbaya sana. Haya maeneo yote yakishawekewa utaratibu mzuri, miundombinu ikakaa vizuri, basi katika haya yote tunayoyazungumzia, yanaweza yakatekelezwa vizuri na yakaleta matunda kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuimarisha kilimo ili viwanda tunavyovizungumza hivi viweze kuzalishwa katika maeneo husika ili mali ipatikane ya kutosha. Ukiangalia nchi yetu inatumia gharama kubwa sana hususani kwenye kipindi hiki cha njaa, lakini ukifuatilia kwa undani zaidi, utakuta ni Serikali haitekelezi wajibu wa kupeleka fedha au kuimarisha watendaji kwa maana ya Maafisa Kilimo katika maeneo husika zikaweza kuzalishwa malighafi za kutosha katika maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia Nyanda za Kusini, utakuta mbolea inaenda muda muafaka, pembejeo zinaenda muda mufaka, lakini leo tunakotoka katika Majimbo yetu, unaweza ukakuta tunavyoongea mpaka leo hata pembejeo hazijafika katika maeneo husika, tayari mkulima yule ataathirika tu kwa namna nyingine na ataanza kulia Serikali. Basi ifike muda muafaka mambo haya yaweze kutiliwa nguvu na kufanyiwa kazi haraka iwezekanavyo, ili wananchi waweze kufaidika na kasi ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu Mheshimiwa Rais alipokuwa akifanya kampeni, alitoa ahadi mbili, barabara ya kutoka Budalagujiga kwenda Mwabasabi, kwenda Nanga na akatoa ahadi ya tatizo la machungio katika vijiji vinavyoishi kando kando mwa mpakani, vijiji hivyo ni Nyantugutu, Pijulu, Mwaswale, Mwamtani na Kuyu, vyote hivyo kuna changamoto kubwa katika maeneo husika. Ningeiomba Serikali kwa ahadi ya Mheshimiwa Rais, nayo iweze kufanyiwa kazi ili wanachi hao waweze kuendelea kuamini na kasi ya utekelezaji ya awamu ya tano.
Mheshimwa Mwenyekiti, tunayo changamoto nyingine, kuna bwawa katika Kijiji cha Habia, limejengwa mwaka 2006. Takribani ya milioni 700 hadi 800 zimeshapotea pale, hakuna chochote kinachoendelea, ukiuliza wakandarasi walitoka Dar es Salaam, hela ile imepotea ukifika pale kwenye site unaletewa kitabu na mtu amebaki pale, kuendelea kusubiri Serikali inasema nini. Nimuombe Waziri wa Maji, jambo hili alitolee majibu, kwa sababu wananchi wa eneo hilo, walitoa eneo lao, lakini hakuna faida yoyote wanayoipata na matokeo yake watu wanapoteza maisha katika eneo lile husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali ya Chama cha Mapinduzi iendelee na kasi iliyonayo, kwa kutekeleza ahadi wanazozisema na kuzifanyia kazi papo kwa hapo. Nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista Mhagama, alikuja katika Wilaya yetu, siku hiyo hiyo akaelezwa kilio cha wananchi na akatoa majibu na hivi sasa wananchi wale walipata alichokiahidi mahindi tani 400, hongera sana Mama, chapa kazi. (Makofi)
Ninamshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya, alitembelea katika kituo chetu cha Nkoma, nadhani hatua zimeshachukuliwa na inaendelea kufanyiwa kazi, hongera sana endelea na moto huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya na Mkoa wetu wa Simiyu ni mpya, bado hatujaungana na Mikoa mingine kwa maana ya lami, ninaomba sasa kilometa 52 zinazotoka Bariadi kwenda Maswa - Migumbi nazo basi Mkandarasi apatikane ili wananchi waweze kuuza mazao yao kwa bei nzuri zaidi. Ukizingatia Wilaya yetu na Mkoa wetu, ni miongoni mwa Wilaya zinazolima kwa wingi sana. Mfano hivi sasa tunavyozungumza choroko zimeshaanza kuuzwa lakini barabara ni mbovu, kwa hiyo mwananchi ataendelea kupata bei za chini. Lakini yote haya yakiwekwa vizuri tunaweza tukafanya kazi kubwa na nzuri zaidi ikawa na matunda na majawabu ya haraka zaidi iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa uvumilivu uliouonesha leo, kweli umedhihirisha kwamba wewe ni Mtemi, umevumilia vya kutosha na hatimaye umetoa majibu, hongera sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja ya Hotuba ya Mheshimiwa Rais
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hotuba ya Bajeti ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kukupongeza kwa kazi nzuri unayoifanya ambayo Watanzania wote na Wabunge wa CCM tunaamini kazi yako ni nzuri sana, kama jina lako lilivyo Tulia, uendelee kutulia kama ulivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza ku-declare interest kwenye upande wa viwanda. Nianze kusema tunapozungumza katika Serikali yetu ya Awamu ya Tano kuhusiana na suala la viwanda kwa ujumla. Tunavyo viwanda, tulikuwa navyo vingi vya pamba pamoja na viwanda vya nyuzi. Katika Bajeti ya Waziri wa Fedha, ukiitafakari na kuifuatilia ni nzuri sana imeonesha maeneo mbalimbali. Nizungumzie suala la pamba na wafugaji pamoja na samaki katika Kanda yetu ya Ziwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kodi iliyopunguzwa ni shilingi 450,000 ukurasa wa 89 na shilingi 250,000, lakini vilevile tunategemea sisi watu wa pamba bei ya soko liko nje, tunajaribu kuangalia mali ambayo iko hapa nchini ambayo wanunuzi wake wako hapa, tayari moja kwa moja panakuwa na kodi kubwa. Mfano mashudu unapoyapa kodi tayari unaongeza gharama kubwa na anayefanya hii biashara ya mashudu ni mtu mdogo wa kawaida, muuza kuku na wafugaji wadogo wadogo, tayari wanaongeza bei ya pamba inaongezeka kupata bei nzuri angalau mkulima, ni kwa sababu control hatuna ya bei ya soko la pamba. Niiombe Serikali ijaribu kuangalia sana kwa mapana zaidi kuhusiana na suala zima la viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye upande wa alizeti, ukipita barabara ya kutoka Singida unaenda Shinyanga utakuta wananchi wameshaji-organise pale wanauza mafuta yale. Lakini Serikali lazima ifike mahali itazame ni namna gani iwasaidie na hawa wakulima wadogo wadogo ili ile mali iweze kuzalishwa vizuri zaidi, iingizwe kwenye soko, i-compete na masoko mengine, lakini hivi sasa inaangaliwa tu, hakuna jitihada ambazo naona kama zinafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile lazima tujipange kuangalia viwanda vyetu vidogo vidogo; mfano viwanda vya SIDO, mimi kwangu kule kwenye Jimbo langu la Itilima ninalo eneo kubwa la SIDO, lakini sijawahi kuona Serikali imekuja kutembelea na kupata mawazo katika eneo lile husika lakini kila siku tu tunakutana tunazungumzia viwanda. Niombe sana Serikali ya Awamu ya Tano iweze kufanya kazi hiyo ili iwafikie wahusika tuweze kuboresha viwanda vyetu na wananchi waweze kupata bei nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunazungumzia habari ya viwanda na vingine. Wenzetu wanaoendelea kwa kasi sana mfano kama Wachina, ziko Benki za Maendeleo ambazo zina-finance wawekezaji, lakini leo nchi yetu hii ukiitazama vizuri sana utakuta gharama ziko kubwa, mtu akitaka kuingiza kiwanda lazima atachajiwa kodi na anaenda kuwekeza zaidi ya miaka miwili, mitatu ndiyo ataanza kupata profit. Moja kwa moja inakuwa ni gharama kubwa katika uendeshaji na hawezi kuendesha kiwanda hicho husika kwa asilimia 100, matokeo yake ni hasara hata fit katika competition ya biashara katika nchi zingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia kuimarisha uwekezaji wetu wa ndani, mimi niiombe Serikali iweze kujua na kufuatilia ni kwa nini wawekezaji wetu wa ndani kila mwaka wanashuka chini, lazima kuna sababu za msingi ambazo zinasababisha. Ukiangalia nchi yetu wakati inapata uhuru, Mwalimu Nyerere yuko nayo kuna vitu vingi ambavyo viliachwa katika nchi hii. Kulikuwa na Musoma, kulikuwa na Mwanza MWATEX, kulikuwa na Tabora, kulikuwa na Urafiki, kulikuwa na Mbeya; zote zile hazifanyi kazi lakini kila mwaka tunapokutana tunaposikia bajeti, tupo wadogo mpaka tumeingia humu Bungeni tunasikiliza mipango, mipango. Ningeomba sasa kwa sababu Waziri wa Fedha ni Mpango, mipango hii sasa ifanane na jina lake, aweke mipango mizuri ili tutoke hapa tulipo tusonge mbele kuleta maendeleo katika nchi yetu na Taifa letu kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie suala la Benki ya Kilimo. Serikali imefanya jambo jema la kuhakikisha inaweka Benki ya Kilimo, sasa tuiombe nayo hii Benki pamoja na msimamizi wa Serikali ambaye ni Waziri wa Fedha awahamasishe sasa watoke mjini waende vijijini. Waende kwenye mikoa ambayo inazalisha siyo kuja kuendelea kulalamika na kuomba fedha hata zile ambazo Serikali imeshatenga bado hazijafanyiwa kazi. Tukifanya hivyo tutakuwa tunawajenga wakulima wetu kuweza kujua jinsi ya matumizi mazuri ya benki na vitu vingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie katika suala zima la ufugaji. Lazima tufika mahali tutambue kwamba ufugaji ni nini na unaingizaje pato katika nchi yetu. Tunapozungumzia ufugaji nao wanahitaji watengenezewe mazingira ambayo ni mazuri na ni salama ya kuweza kunufaika na maeneo yetu.
Tunatambua kabisa katika nchi yetu tunaamini kabisa kwamba tunahitaji hifadhi na kadhalika, juzi Mheshimiwa Waziri wa Maliasili alikuwa anajibu swali langu alisema vijiji vinavyopakana na kandokando ya hifadhi zinapata asilimia 25 ya fedha zinazotozwa, siamini kama zile fedha kweli zinaenda tofauti na hela tu ndogo, nitaomba Mheshimiwa Waziri nitamtafuta kwa muda wake anielekeze ni jinsi gani kwa sababu naamini hela zinazokuja ni kidogo sana wala haziwezi kuwasaidia wananchi katika maeneo hayo wanayoishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze Benki ya Maendeleo. Benki ya Maendeleo ndiyo uti wa mgongo wa nchi yetu. Kama tunataka tujenge viwanda na kama tunahitaji tuwekeze katika maeneo mbalimbali, hii benki ikiwezeshwa na ina wataalam inaweza ikafanya kazi kubwa, nzuri ya kuingiza fedha nyingi bila kutegemea kodi tu kwa sababu itazungusha na wale watu wawekezaji watakuja kukopa katika benki yetu hii na itaweza kuzalisha fedha nyingi katika kuleta uchumi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho niishauri Serikali, hii kodi ambayo imewekwa kwenye mabenki, ninavyoiona inaweza ni nzuri kwa sababu tunahitaji tupate kodi, lakini kwa mtazamo wangu na muono wangu na kuishauri Serikali tunaweza tukajikuta tunapoteza deposite nyingi kwenye mabenki kwa sababu kodi itakayotozwa ni hela nyingi sana. Sasa hivi kama una wafanyakazi 300, ukipeleka kwenda kufanyiwa malipo kila mfanyakazi mmoja ni shilingi 3,000 kwa hiyo utakuta watu hawaweki hela kwenye benki wataamua kutumia njia zingine, tayari nchi itaanza kuyumba katika hali ya kiuchumi. Niombe hilo nalo waweze kuliangalia ni jinsi gani ili waliboreshe vizuri zaidi na lengo letu ni kupata mapato mengi ya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie katika Kanda, mfano Kanda ya Ziwa iangalie ni viwanda gani vinavyohitajika katika maeneo yetu. Leo hivi sasa tunazungumza bei ya pamba haieleweki na wakulima nao wanasubiri wauze waweze kupata fedha zile, lakini kila mwaka zao hili linadorora, ukifuatilia zaidi zao hili linaingiza fedha nyingi sana kwa mwaka, mwaka jana tumepata dola bilioni 6.4, lakini hakuna kipaumbele kinachowekwa na Serikali kuhakikisha kwamba hawa wakulima wa zao la pamba tunawasiadiaje kuongeza hizi gharama, matokeo yake zinaongezwa tu kodi katika maeneo husika na imefika mahali Serikali hata ruzuku ya pembejeo haipeleki, kwa mwaka wa jana haikupeleka hata senti moja, wakulima wenyewe wanaendelea kujiendesha. Niiombe Serikali ijaribu kuangalia namna gani kuhakikisha inatatua tatizo la bei ya pamba katika maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho tukitaka tuende vizuri, zao hili la pamba linaweza likajiendesha vizuri sana, zikipungua kodi ambazo hazina msingi, ambazo zinazosababisha kuongezeka kwa bei, kwa sababu hatuwezi tukasema kwamba tuzuie kodi, lakini lazima tuangalie kwamba inaingiza kiasi gani kwenye nchi dola za kigeni na asilimia kubwa nchi inatumia fedha za kigeni nyingi, kwa sababu mahitaji mengi hatunayo hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie ni jinsi gani itasaidia katika eneo hili ili tupunguze malalamiko katika maeneo na ipunguze hizi kodi ambazo hazima maana. Kweli naiomba Serikali suala kabisa la mashudu watoe kodi haina sababu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia 100.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya wakulima na mimi nikiwa kama mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuipongeza Serikali, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na wataalam, kazi yao inaonekana. Kwa miaka miwili tumeona bei za mazao yetu zikiongezeka. Pamoja na hilo, ziko changamoto ambazo tunahitaji wazitatue kama Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la tozo kwenye mazao yetu, zile tozo zinazopunguzwa moja kwa moja zinaongeza thamani ya bei ya mkulima. Nimepata tabu kidogo Waheshimiwa Wabunge wanasema inamsaidiaje mkulima. Ni suala la kujiuliza kwa sababu mfanyabiashara siku zote yeye hapati hasara, gharama zote anampelekea mkulima. Kwa hiyo, tunapojaribu kuchangia kwenye suala la kilimo tuwe makini sana pale tunapoishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana unakuta kwenye zao la pamba kuna VAT na asilimia 70 ya wakulima wanaotarajiwa kuwezesha viwanda na vitu vingine wanatokana na kilimo. Sasa utaona asilimia 70 hii ya wakulima wote wanapelekewa VAT na akipelekewa VAT automatically ile VAT itakwenda kumpunguzia mkulima, kwa hiyo, utaona bei zinakuwa chini. Ndiyo maana unakuta mazao mengi wakulima wanakuwa wanayakimbiakimbia kuyatekeleza, wanaibua wao wakulima wenyewe kwa maarifa yao lakini yakishaibuliwa inakuja kodi mbele yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Serikali mambo haya ya msingi tuyaangalie, huwezi kuweka VAT kwenye pamba. Mashudu kwani mfanyabiashara mdogo yule ambaye angenunua yale mashudu kwa ajili ya vifaranga vya kuku na vitu vingine vingeendelea kufanyika umeshamwekea kodi hataweza kununua na hivyo bei ya pamba haitapanda katika maeneo yale. Kwa hiyo, utakuta bei zinaendelea kushuka kwa sababu hatuwezi ku-control masoko haya tunatarajia kutoka nchi za nje. Kwa hiyo, naomba suala hili la mazao hususani zao la pamba mwangalie sana kodi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kusema ametoa kodi kwenye pamba, Mwenge sio kodi, ni makubaliano kati ya DC na ginneries husika. Suala la msingi hapa ni kwamba toeni VAT kwenye suala hili ili bei za wakulima ziendelee kuongezeka na zikitolewa tutapata fedha nyingi za kigeni lakini tutapata ajira nyingi na viwanda vitaendelea kufanya kazi katika eneo letu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la mbegu. Kwenye suala hili la mbegu watafiti wetu wanaendelea kutafiti vizuri tu kwa muda mrefu lakini ukijiuliza, mfano, nataka nizungumzie suala la pamba, kuna mbegu ya UK91 imeshapitwa na wakati. Ndiyo maana siku zingine Wabunge tunauliza kwa nini mbegu hazijaota, hii ni kwa sababu zimeshapitwa na wakati na watafiti na wataalam wanalifahamu hili hata mfumo wa kuzipitisha hakuna, zinakuwepo tu ili mradi lakini GOT yake ni kidogo asilimia 32 inayosababisha hata bei zenyewe za pamba zisipande. Kuna hii UK08 ikisimamiwa vizuri, ikizalishwa vizuri katika maeneo husika tuna uhakika tutazalisha GOT asilimia 40 ambayo itakuwa ni average kubwa sana na tutapata fedha nyingi za kigeni katika maeneo yetu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mifuko ambayo ilianzishwa ya CDTF ilikuwa na wadau watatu, Serikali, wakulima pamoja na wafanyabiashara wenye mfuko husika. Kwa muda mrefu sana fedha hii imekuwa ikitumika nje ya utaratibu badala ya kumnufaisha mkulima anakuwa anafanya double payment, amechangia kwa mwaka huu na mwaka unaokuja anaambiwa kuchangia halafu mwisho wa siku hapati pembejeo. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwa mwaka huu ambao tunaumalizia maeneo mengi yameathirika sana kwa sababu ya pembejeo hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mfumo huu ulivyoanzishwa kulitengenezwa kitu kinaitwa pass book kwamba mkulima alikuwa anaweka benki yake, benki hii akienda kuchukua dawa ina maana apewe bure lakini matokeo yake mkulima huyu amekuwa akitozwa. Nimwombe Mheshimiwa Waziri hii pembejeo ya mwaka huu awatangazie wakulima na wananchi wa Tanzania nzima hususan mikoa inayolima pamba kwa sababu ni pesa zao walizozichanga, hakuna sababu ya mtu anakuja anasema anafanya kilimo cha mkataba na kilimo cha mkataba hiki tayari pembejeo zile alishachangia mwananchi. Kwa hiyo, hizo anatakiwa apewe bure ili aweze kujiendesha kwa msimu unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niombe kwenye suala zima linalohusiana na suala la kilimo cha mkataba tungetafuta jina lingine, sio kilimo mkataba. Hii ni kwa sababu unaposema mkataba unapomaliza mkulima atakwambia nataka niuze bei hii na sisi hatupangi bei, tunategemea mataifa makubwa yanavyopanga bei ndiyo tunashusha gharama zetu na kadhalika ndiyo tunapata bei sahihi. Kwa hiyo, naomba litafutwe jina lingine, dhana ni nzuri ambayo itaweza kuboresha na kuleta tija kubwa katika uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona ukurasa wa 34 wamesema wastani wa uzalishaji umeongezeka kutoka 728 kwa hekta kwenda 925. Napata tabu kwa sababu mwaka jana takwimu walizotuletea walisema kwamba takribani hekari milioni moja za pamba zimelimwa. Kwa takwimu hii ukiizidisha tungepata milioni 328, matokeo yake kwa mwaka jana tumepata milioni 120 tu. Kwa hiyo, utaona hizi takwimu ni za kukaa na kujifungia na kubumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana suala hili hasa la utafiti litiliwe mkazo na waangalie ni jinsi gani itakayoweza kusaidia. Haya mambo tunayazungumza sana, wakulima wanayazungumza lakini tuna tatizo la wataalam kwa maana ya Maafisa Kilimo, hatujui wanawajibika kwa nani, nalo hili ni tatizo kubwa. Kwa hiyo, tunamwomba Waziri aweze kukaa na kujua mamlaka haya husika, huyu mtu anawajibika wapi, bodi yupo peke yake, atazunguka na pikipiki yake katika Wilaya nzima lakini pale kwenye Serikali kwa maana ya TAMISEMI kuna Afisa Ugani kila Kijiji, Kata na kila maeneo lakini hawa watu hawawajibiki, wanawajibika kwa nani? Mwisho wa siku inapotokea sasa Halmashauri imetengeneza mapato ndiyo watu wa kwanza kuingia kwenda kutoza kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili ni tatizo na lazima tuliangalie kwa mapana Waheshimiwa Wabunge tujaribu kusaidia kwamba mifuko yetu hii na bodi zinazoundwa hizi ziweze kufanya kazi yake vizuri lakini ziweze kuisaidia Serikali. Waziri kwenye suala zima la Bodi ya Pamba sasa hivi ni mwaka wa tatu Bodi ya Pamba haina Board Members wake ndiyo maana tunakosa mambo mengi maeneo yetu kwa sababu hakuna ushauri. Mnakutana na wataalam wale wale mkirudi hakuna jambo jipya litakaloendelea kupatikanika katika maeneo yetu. Naomba hilo nalo Mheshimiwa Waziri ajaribu kuliangalia, hii bodi itatengenezwa lini na vitu gani vifanyike ili mambo yaende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nimpongeze Mkurugenzi Mtunga na Waziri kwa sababu mmeendelea kutengeneza mfumo mzuri wa bei. Nina imani na mwaka huu bei zetu zinaweza zikawa nzuri. Ombi kubwa kwa Serikali toeni hizi kodi na wananchi watajiendesha wao wenyewe. Haya mambo tunazungumza, leo tuna asilimia tatu tu ya kilimo lakini mwananchi huyu anaendelea tu kuhangaika kule lakini bado hatujataka kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba sana hasa kwenye suala zima la mbegu tunajua kule Simiyu, wameanzisha na Meatu ni jambo jema na maeneo mengine tujipange kuhakikisha tunaweka utaratibu mzuri. Vilevile wako wakulima wazuri tu ambao wanaweza wakafanya
kazi hiyo kwa kuwaelimisha wengine. Nashauri angalau kila kijiji kuwe na wakulima wawili ambao watakuwa ni sehemu ya mfano, watu watafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kwenye suala la la mbegu za mahindi wakati zinakuja watu walikuwa wanalalamika lakini sasa baada ya kuona uzuri wa mbegu zinavyozalisha watu wanaenda kununua wenyewe tofauti na kutumia nguvu kubwa na fedha nyingi. Nina imani wakulima wa kanda zetu kule wakishajua jambo wao wenyewe hujiongoza. Unaweza ukasema wakati mwingine hata kilimo wanaweza wakawa wanakwamisha, wanawapa matumaini makubwa, matokeo yake hata mbegu hawaleti. Kwa hiyo, tufike mahali tusiwe tunatoa matumaini kwa wananchi wetu ambapo wanatarajia kwamba kuna kitu fulani kinakuja, pembejeo inakuja mwezi wa Nne au wa Tano kitu ambacho inakuwa muda wake umeshaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nashukuru sana, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hotuba hii ya wananchi wanyonge walioko vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mitatu mfululizo katika zao la pamba tumekuwa tukipata bei nzuri. Mwaka 2016, 2017 na 2018 na tumevuka kiwango mpaka tumefanikiwa kuzalisha takribani kilo 600,000, haya ni matarajio ambayo tunayatarajia. Hii ni kwa sababu wananchi wamehamasika kwa sababu ya kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uzalishaji wa zao hili la pamba, linaweza likaipatia nchi kipato kikubwa sana. Kwa mwaka huu wa fedha tunatarajia kuwa na Dola za Kimarekani takribani 342 lakini kadri tunavyokwenda na taratibu ambazo Serikali yetu ya Awamu ya Tano ilielekeza, namshukuru Mbunge aliyemaliza kuchangia Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba tuwe na ushirika kwa ajili ya kukomboa wanyonge, nataka nikuhakikishie ushirika unaotengenezwa siyo ushirika ambao tunaufahamu, ni ule ushirika wa miaka yote ya nyuma. Ni watu ambao walishachoka tangu miaka 23 na mwaka huu kama tutawakabidhi huu muziki wakulima wetu wataendelea kupata adha kubwa sana. Ningeiomba Serikali ijaribu kutengeneza upya mfumo wa kuhakikisha kwamba zao hili la pamba linanunuliwa vizuri na kwa umakini mkubwa zaidi. Hata go-down walizonazo zilishauzwa, ushirika uliobaki kule ni ushirika ambao ni hoi bini tabani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unatoka katika Wilaya ya Bariadi unayo majimbo mawili, Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Vijijini, ushirika uliopo katika kijiji chenye watu 2,000 kuna washirika watatu, wanne na leo tunataka kwenda kuwakabidhi fedha za wakulima wetu. Niiombe
Serikali sikivu ya Chama cha Mapinduzi, kilio hiki iende ikakifanyie kazi upya kuliko hivi sasa ndiyo wanahangaika kule vijijini wanaunda vikundi na hizi ni fedha za watu na mabenki inabidi benki hizi zirudishe fedha na kipato cha ndani kiendelee kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala zima la pembejeo. Tumeshuhudia mwaka huu Mheshimiwa Waziri amefanya kazi nzuri pamoja na watendaji wa Bodi ya Pamba kwa kuhakikisha ametutoa tulipokuwepo na kutufikisha hapa tulikofikia. Matarajio yetu tukiendelea kusimama vizuri na kuimarisha zana zetu katika maeneo yetu ya kilimo cha pamba, katika hotuba yake amesema ifikapo mwaka 2020 tutafikisha tani 1,000,000, naamini bei zikiendelea kuwa nzuri na pembejeo zikiwa za kutosha ifikapo mwaka 2020 tutazalisha tani milioni 2.4. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu mikoa inayolima pamba ni 17, tunazo wilaya 56 utaona tu kwamba hata uzalishaji tulionao kwa mwaka huu tumepiga hatua. Ukigawanya wastani wake ni kama kila wilaya imezalisha tani 10 ambapo tukisisima sasa jukumu hili tukalibeba wote Serikali pamoja na Wabunge kwa kuhamasisha na kuunda AMCOS zilizosajiliwa kwa mwaka huu uzalishaji utaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Waziri Mkuu kutoa agizo Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kwenda kuunda vikundi kilichofuatia ni Mrajisi kwenda kutengeneza ushirika wake wa miaka 20 ambao umefilisi wananchi wetu na bado watu wanauchukia hata sasa hivi ukisema ushirika wanakimbia. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuliangalia suala hili kwa mapana zaidi, zana ni nzuri lakini si nzuri kwa kipindi ambacho tunakitarajia hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 146, hapa napata kigugumizi kusema, ametuandikia ameamua kufuta Mfuko wa Wakfu wa Kuendeleza zao la Pamba lakini kwenye kukotoa huku kuna Sh.100, sasa angetupa majibu tunafanya kitu gani? Hizi fedha zikienda kwa mkulima moja kwa moja bei zinaongezeka. Kwa hiyo, naomba sana hili suala la pembejeo Waziri ahakikishe linakuwa katika mipango mizuri ili wakulima wetu wasiendelee kupata adha ambayo wanaendelea kupata kwa mwaka huu tunaoumaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu tutakapoweka usimamizi na uzalishaji mzuri wakulima wetu wa pamba hawasukumwi kwa sababu ni wajibu wao na ni biashara yao lakini tunavyotaka kwenda tunaweza tukatengeneza mazingira ya kuua zao la pamba na litafia hapa Dodoma. Kwa mwaka 2020 tunarajia kuvuna tani 1,000,000 lakini kwa mfumo ambao ameuleta Mheshimiwa Waziri hatutafikia huko, wakulima wataacha kulima kwa sababu hii miti wanalima kwa mwaka, wanakata wanazalisha tena upya. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atafute mfumo ambao ni mzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo linatuletea masikitiko makubwa sana. Sisi kule kwetu tulikuwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha SHIRECU lakini baada ya Ofisi ya Mrajisi kuingia pale alitengeneza madudu mpaka na go-down zetu kubwa zilizokuwa maeneo ya Dar es Salam ziliuzwa lakini leo Mrajisi huyu amerudi tena na mifumo ambayo badala ya kuishauri Serikali alete utaratibu mpya utakaokuwa na tija kwa wakulima ameleta system ileile ambayo imewatesa wakulima wetu na imewakatisha tamaa. Watu wengine, Mwenyekiti utakuwa shahidi wakati wa kampeni za kuomba kura, watu walikuwa wanakuomba malipo yao ya pili. Kwa hiyo, naomba jambo hili tulichukulie katika misingi mizuri ambayo ina tija lakini kubwa zaidi ni kuweka mifumo itakayokuwa rafiki na wakulima ambao wanazalisha bila kusukumwa na kwa moyo mzuri na ni kwa sababu wanapata pesa nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshauri Waziri aweke mpango mzuri utakaotuwezesha kupata pembejeo na mbegu bora. Niwashukuru sana watafiti wetu wa Ukiliguru kwa sababu kwa mwaka huu fedha tunaenda sasa kuingia kwenye mbegu za asili ambazo wamezizalisha, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nishauri tuendelee kutunza mbegu zetu za asili. Hili jambo tusipoliangalia ni tatizo na janga kubwa. Wakulima wetu wanahamasika sana kulima, nimeona humu ndani kwenye kabrasha hili kuna mikoa mipya imeanzishwa. Mikoa mipya iliyoanzishwa kama mfumo wetu hautakaa vizuri, nataka nikuhakikishie tutapata madhara makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi tunao, mwaka 2008/2009, Serikali ya Awamu ya Nne ilitoa fedha kwa ajili ya kufidia wakulima takribani shilingi bilioni 2 lakini zile fedha zilitumika ndivyo sivyo. Leo hii Serikali ya Awamu ya Tano tangu iingie madarakani bei zimeendelea kuongezeka kila siku, sasa kuna mdudu ambaye ameingia huyu sijui katoka wapi. Naomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kwa hili atuwekee utaratibu utakaokuwa rafiki kwa wananchi wetu na tusiwe na maswali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna meseji kibao za wananchi wanalalamika kwamba Bunge lilitangaza tarehe 1 lakini mpaka leo hakuna na wamefungua kijiji kimoja pale Igunga kilo 3,000 zilizonunuliwa, hakuna mtu yeyote aliyeingia mule ndani lakini hata maandalizi hayapo, hata msimamizi wa Bodi anapata wakati mgumu. Mrajisi ana mwongozo wake, Bodi ina mwongozo wake, mwisho wa siku tunashindwa kuwaweka wananchi wetu katika mazingira yenye kuleta kipato kikubwa. Nchi hii tumekubaliana kwamba lazima tuwe na uzalishaji mkubwa ili tukidhi mahitaji ya wananchi wetu. Ukizalisha mbegu nyingi tena tutapata mafuta mengi, tuna alizeti, mawese na vitu vingine lakini wananchi watalima pale ambako hakuna usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba amesema amejipanga kuhakikisha kwamba vyama vya ushirika vinakusanya pamba halafu mnunuzi aende kununua. Ni mwananchi yupi atakayepeleka kwenye vyama vya ushirika ambavyo watu wamekosa imani, hiyo ni kazi ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali jambo hili iliangalie kwa mapana zaidi na tuliwekee utaratibu mzuri utakaokuwa na tija kwa wananchi wetu. Hili jambo wakilipokea itakuwa ni vizuri zaidi kuliko hivi sasa hata ile iliyowekwa kwa mwaka huu Sh.12 inaenda kuimarisha union, kwa hiyo, mwananchi huyu ataendelea kupata shida tu. Pangekuwa na mifumo mizuri kule kijijini kama alivyoelekeza Waziri Mkuu katika kikao chake cha Wakuu wa Mikoa kwamba tunataka hizi AMCOS zimilikiwe na wenyewe lakini mliporudi ninyi kwenye sheria na utaratibu wenu mkasema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, hotuba muhimu sana kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mimi nitaendeleza tu kwa yale ambayo umezungumza kwa sababu mimi ni mkulima na mfugaji, nitazungumzia sana kuhusiana na pamba. Pamba inazalishwa katika Mikoa 17 na pamba inazalishwa katika Wilaya 56; kwa wale ambao hatuna biashara zingine kwenye Wilaya zetu tunategemea mapato kutokana na hilo zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Simiyu inazalisha 60% ya pamba kwenye nchi hii na ndiyo maana Serikali Awamu ya Tano ilipokuja ikaona suala la pamba ikaja na mkakati wa kutengeneza kiwanda cha vifaa tiba pale Wilayani Bariadi. Sasa mkakati huu umekuwa wa muda mrefu takribani tangu mwaka 2016 leo ni miaka minne, Serikali tunakwama wapi? Lakini ukiangalia kwenye hoja za CAG katika mradi huo imetumika shilingi milioni 900 kwa ajili ya kumaliza upembuzi na vitu vyote kwenye mradi huo wa Simiyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningeomba tu Serikali kwenye mipango mikubwa hasa kwenye mikakati ya kimkakati kwenye zao la pamba hususan kwenye mkoa wetu wa Simiyu na mikoa mingine 17 ambayo nimeitaja. Mradi huu utakapokamilika utasaidia sana kwa wakulima wa pamba katika mikoa hiyo na wilaya hizo zinazozalisha na hii itaongeza tija kwenye uzalishaji wa pamba na itaongeza tija kwa wakulima wetu, lakini itaongeza ajira kwa vijana ambao wanamaliza shule, lakini na sisi vijana ambao tunaendelea na biashara zetu tutaendelea kuziendeleza vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri ningekuomba sana suala hili liwe kipaumbele kuhakikisha kwamba taasisi yako ya viwanda na biashara kusudi ambalo linalotarajiwa lifanyike na wananchi tuone kwamba kweli haya yanayozungumzwa na Serikali yanafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo viwanda vya ushirika, Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilisema tuwe na ushirika, ni jambo jema kuhakikisha tunamkomboa mkulima wetu ambao wanaushirika hawa wakiwa jumuiya ya pamoja wataungana na kukisemea kile ambacho wamekizalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini changamoto inayokuwepo sasa badala ya kwamba ushirika hawa waendelee kujiimarisha hatua inayofuata ushirika anakuwa sasa dalali wa kwenda kuwatumikia wenye viwanda private ambapo mimi naamini kabisa wangeanza na hatua ya kwanza tuko na viwanda. Hayati Mwalimu Nyerere alitengeneza nchi hii kimkakati, kila mkoa kulikuwa na kiwanda cha nyuzi, kulikuwa na viwanda vya pamba mfano ukiangalia kwenye mkoa wetu wa Simiyu tuna viwanda takribani viwanda sita vya ushirika lakini hakuna mkakati hata mmoja ambao Serikali inauleta sasa tunaenda kuzalisha kuweza kusimamia kiwanda kimoja cha ushirika tukiboreshe ili kusudi sasa uzalishaji wa pamba washindane na hawa washirika na private sector.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachofuatia Serikali ni kuja na mawazo, wewe private sector fedha zako utapeleka pale kwenye ushirika watakununulia pamba, sasa unajaribu kujiuliza kwa njia ya harakahara.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Njalu naomba ukae. Kuhusu Utaratibu.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni ya 68 naomba nisome.

MWENYEKITI: Isome.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa majadiliano Bungeni au kwenye Kamati yoyote ya Bunge, Mbunge hataruhusiwa kuzungumzia jambo lolote ambalo yeye mwenyewe ana maslahi binafsi nayo ya kifedha, isipokuwa baada ya kusema jinsi anavyohusika nalo na kutaja kiwango cha maslahi hayo na kwa sababu hiyo itakuwa ni lazima kwa Mbunge yeyote anayetaka kuzungumzia jambo hilo Bungeni au kwenye Kamati yoyote ya Bunge kusema kwanza jinsi anavyohusika na jambo hilo na kutaja kiwango cha maslahi ya kifedha aliyonayo kuhusiana na jambo hilo kabla ya kuanza kuzungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hili, kwa sababu imekuwa ni udamaduni hapa Bungeni lakini imenibidi niseme tena sasa kwa sababu anayezungumza ni rafiki yangu, mosi; yeye ni mkulima wa pamba, pili yeye ni mfanyabiashara wa pamba, ananunua pamba kutoka kwa wakulima na tatu yeye ana ginneries za pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu kanuni zetu zinatupa huo utaratibu nilikuwa nashauri tu umpe mwongozo ili kutuwezesha tusiende hatua za mbele zaidi za kikanuni ambazo nadhani ni kali zaidi. Ili vilevile na Wabunge wengine siku nyingine wakiwa wanachangia masuala ambayo wana maslahi nayo binafsi kuanza wa-declare baada ya ku-declare sasa waendelee na mambo mengine, tunafundishana tu ili mwenendo mzuri wa Bunge uweze kwenda nashukuru. (Makofi)

MWENYEKITI: Sawa Mheshimiwa Halima ametoa Kuhusu Utaratibu kwa Mheshimiwa Njalu, lakini nafikiri Mheshimiwa Njalu anaelewa vizuri utaratibu huo na angekuwa na maslahi ya kifedha ambayo yanatakiwa kikanuni angeweza ku-declareinterest kwa vile hakusema na haku-declare ina maana hana maslahi ya kifedha. Tunaomba tuendelee. (Makofi)

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru japokuwa alitaka kunichokoza, unajua ndugu yetu naye ana changamoto zake, nimemsamehe. (Makofi/ Kicheko)

Mimi nazungumza kadri ya maslahi ya nchi yetu na ningekuwa nimetaja maslahi yangu binafsi nisingeeleza haya yote kwa sababu lazima ufahamu unapokuwa kwenye biashara ni kuzungumzia masuala yako binafsi, lakini nimezungumza mjadala wa umma, nimezungumza Mikoa 17, Wilaya 56, nimezungumza habari ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni sehemu ambayo nafaidika nisingeelezea hayo, kwa hiyo ni suala la kujifunza na kuendelea naye kuelewa kwamba tunajifunza kitu gani, lakini na mimi nimeshakuwa senior humu ni mwaka wa saba niko Bungeni humu sasa, kwa hiyo, suala ambalo lazima ujuwe una form one hapa wala siyo njuka. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi zetu za Serikali mfano; TIRDO tulitembelea sisi kama kamati tumeona ufanisi wake, lakini bado uwezo hawajajengewa kifedha. Mimi ninaamini kabisa yote tunayoyazungumza haya TIRDO tukiijengea uwezo wanauwezo mkubwa sana wa kutengeneza viwanda vidogo vidogo ambavyo vinazalisha alizeti, mpunga na kadhalika. Kwa hiyo, haya yote tukiyachukuwa tunaweza tukapiga hatua na nchi yetu ikaongeza ajira kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niendelee kusema kwamba suala hili ni muhimu sana kwa nchi, lakini vilevile suala hili ni muhimu kwenye kodi kwa sababu unapotengeneza wafanyabiashara ndiyo unazalisha kodi unazalisha walipa kodi wengi nchini hasa sehemu sekta ya viwanda na biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningekuomba sana Mheshimiwa Waziri, nadhani Mheshimiwa Waziri ulitembelea kule Katavi uliona kwamba watu wanavyowekeza kwenye viwanda kwenye mikoa hii mipya, kwa hiyo, ni imani ya kwamba shughuli zikienda sambamba itatusaidia sana na wewe Mheshimiwa Waziri na Serikali sehemu kubwa ninyi ni kuhakikisha wafanyabiashara mnawawezesha kwa miundombinu, mnawezesha kila jambo ili kusudi nchi yetu iendelee kufanya mapato ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bunge lililopita nilishawahi kusema kwamba Waziri wa Viwanda na Biashara, Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara hawa ni sehemu kubwa sana ya kuiwezesha Serikali kukusanya mapato yake makubwa sana bila hata bugudha yoyote ile, lakini kulingana tu na sera sijui mipango au kwa sababu ni kutimiza wajibu, kila mtu akiamka anaamka na analolifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko changamoto nyingine moja kwenye suala la nchi zetu hizi wanazofanya biashara kwa kuingiliana mfano Zambia na Tanzania kuna sheria imepitishwa Zambia asilimia 50 wanataka wao mzigo wabebe Wazambia kupita malori yao, lakini asilimia 20 ibebwe na Watanzania, asilimia 30 iende kwenye train. Sasa jambo hili siyo afya sana. Sasa kwenye mjadala huo hatujui umeanzaje mpaka Waziri wa Zambia akafika mahala hakatoa huo waraka wake kwenye nchi zetu za Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeshauri na lenyewe Mheshimiwa Waziri ulichukuwe mjaribu kulifanyia kazi ili kusudi biashara hizi zifanyike vizuri zaidi na watu waendelee kupata mapato kwenye nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kumshukuru Waziri wa Viwanda na Biashara kwa hotuba yake nzuri ambayo imeelekeza changamoto za Watanzania. Nitaanza na ku-declare interest kwa maana ya kwamba ni mmiliki wa kiwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia viwanda tunazungumzia viwanda vya aina gani? Sisi wakulima wa pamba tunakotoka tulikuwa na viwanda 77 leo vimebaki 40 na hivi 40 na vyenyewe vipo katika hali tete. Nini mpango wa Serikali kuvisaidia viwanda hivi ili viweze kufanya kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumza na ukifuatilia suala la viwanda kwanza malighafi yenyewe haipo ni kwa sababu Serikali haijaweka kipaumbele kwa mazao yanayozalishwa hapa nchini ili yaweze kuwa na bei kubwa. Kwa mfano, pale Morogoro tunacho Kiwanda cha Ngozi baada ya Serikali kuzuia ngozi zetu zisisafirishwe bei zimeshuka. Leo bei ya kilo moja ya ngozi ya ng‟ombe ni shilingi 400 lakini enzi zile wakati wanasafirisha ilikuwa ni shilingi 1,500, ya mbuzi ilikuwa shilingi 1,000, ya kondoo ilikuwa shilingi 800, leo unazungumzia ya kondoo shilingi 100 kwa kilo na ya mbuzi unazungumzia shilingi 200, kwa jinsi hii tunalindaje viwanda vyetu vya ndani? Ifike mahali sasa Serikali ijaribu kuangalia kwa undani na kwa umakini zaidi ili kuhakikisha mali tunayoizalisha hapa nchini inakuwa na viwanda vya kuzalisha vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ione ni jinsi gani ya kuongeza bei, hili jambo kwa kweli linanipa taabu. Unakuta mazao yetu ya ndani kodi inaongezwa, mfano kama pamba. Mashudu yana kodi, mafuta yana kodi lakini mali inayotoka nje inakuwa haina kodi, unategemea hii mali itapanda kwa utaratibu upi? Ukizungumzia zao la pamba, zao la pamba linajumuisha vitu vingi, utachukua mapumba yale makapi, utachukua mbegu zake utauza lakini kwa hali iliyopo ukigusa kila kitu kina kodi kwa sababu sisi soko la nje hatuli-control hatuwezi kuongeza bei na mkulima bei yake ikiongezeka ni sehemu ya kichecheo kwa wakulima kuweza kuzalisha kwa mwaka unaofuata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Wizara ya Kilimo imezungumza, kwa mwaka 2004 nchi ilizalisha robota 700,000 lakini leo tunazungumzia uzalishaji wa tani 150,000, ni tayari nchi imeingia hasara kwa aina gani? Tumekosa dola lakini vilevile tumekosa ajira kwa vijana wetu. Mimi niiombe sana Serikali, Waziri atenge muda wa kukutana na wenye viwanda hawa ili aweze kuzungumza nao wamwambie ni changamoto za aina gani wanazokabiliana nazo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani nchi inazungumza kila siku masuala ya viwanda lakini bado kuna watu ambao wana viwanda lakini wameshindwa kuviendesha kwa sababu ya mambo mengi. Tuna kiwanda pale Arusha kipya na kizuri kabisa lakini kimeshindwa kufanya kazi. Hata huyu Mchina ambaye yuko pale Shinyanga amefungua Kiwanda cha Nyuzi pamoja na Kiwanda cha Oil Mill haviwezi kufanya kazi kwa sababu ya malighafi na gharama inakuwa kubwa. Kwa hiyo, ifike mahali tuangalie ni jinsi gani tunataka kuwasaidia Watanzania lakini tuangalie ni jinsi gani tunataka tusimamie mazao yetu ya ndani ili kuyaongezea thamani ili wakulima wetu waweze kupata bei zilizokuwa nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mambo mengi ambayo yanasababisha tushindwe kusonga mbele. Ukiangalia mfano mwaka huu tumekosa pamba na mtu anayehusika na viwanda anapaswa sana kusimama kwa sababu ni sehemu yake ili viwanda vyake viweze kufanya kazi. Mwaka huu tuna maeneo mengi ambayo yamesababishiwa hasara na baadhi ya wataalam wa TPRI kwa sababu ya kuleta dawa mabovu hivyo hatuna pamba ya kutosha. Hili jambo lazima Waziri wa Viwanda aliangalie kwa umakini zaidi na kuhakikisha wanakuwa wamoja ili wasukume gurudumu la maendeleo kuhakikisha nchi yetu tunaipeleka mahali tunakokusudia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto nyingine kwenye suala la viwanda. Viwanda vyetu lazima tukubali, kwanza suala la umeme bado halijakaa vizuri, lazima ongezeko la umeme wa kutosha liwepo. Kiwanda unakiendesha ndani ya miezi miwili, lakini ndani ya miezi hiyo miwili utalipa miezi mitatu inayofuata, kama ni bili ya shilingi milioni 100 utalipa miezi mitatu mfululizo, tayari pale yule mwenye kiwanda hawezi kuendelea atasimama tu hivyo hivyo na mwisho wa siku nchi yetu itaingia kwenye matatizo makubwa sana.
Niiombe sana Wizara inayohusiana na jambo hili ilishughulikie kwa umakini zaidi na kuona jinsi gani sasa tunasonga mbele na kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais inayosisitizia suala la viwanda. Viwanda vina changamoto na lazima Mheshimiwa Waziri aingie ndani zaidi, ajifunze zaidi najua ni mtaalam na jinsi anavyojibu yuko shapu kama Mbunge wa Kishapu akiweka mambo yake vizuri tunaweza tukapiga hatua kubwa sana lakini bila kufanya hivyo tutazungmza hapa miaka mitano itaisha na viwanda havitaenda ni kwa sababu mambo hayako wazi tunaelewa kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu walioendelea, kuna nchi kama Bangladesh, ina sehemu tu ya viwanda, kiwanda kimoja kina wafanyakazi 25,000, kila kitu kipo na masaa yote kinafanya kazi lakini sisi Tanzania hapa hatujajipanga vizuri. Hata hivyo, kwa kasi hii ya Awamu ya Tano naamini imejiwekea utaratibu mzuri. Niwaombe sana Waziri wa Kiwanda pamoja na Waziri wa Nishati na Madini muweke kasi kwenye mambo ya umeme kwa sababu viwanda vyetu vina fail, vinaunguza vitu kutokana na mambo mengi. Yote haya tukiyazingatia na kuyachukulia maanani tutapiga hatua na nchi yetu itabadilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mambo magumu sana ambayo tunayaona lakini mambo mepesi sana tukishirikiana na wananchi wetu, tunavyo viwanda vya SIDO. Mfano mimi kwenye Jimbo langu pale Luguru, maana Mwenyekiti wewe ni Mtemi kule, kuna Kiwanda cha SIDO kipo siku nyingi tu. Kile tayari kikitengenezewa utaratibu kinafanya kazi maana majengo tunayo zile teknolojia zipo zinabadilika kila siku tu ni kwenda kutoa zilizokuwepo unaweka mitambo mingine kazi inaendelea, lakini bado sasa tunazunguka na tunazungumza sana. Kama tunataka vijana wawe na ajira ni pamoja na vitu kama hivi tukiviwekea kipaumbele tunaweza tukapiga hatua na nchi yetu tukaipelekea pale panapokusudiwa. (Makofi)
Suala lingine ni alizeti. Sasa hivi pamba inaenda inashuka lakini alizeti sasa nayo imeingia kwenye soko. Nimuombe Waziri wa Viwanda ajaribu kuangalia na kutoa ushauri kwenye Wizara ya Kilimo kwa sababu ni wamoja wanaweza wakaungana wakafanya kazi ya pamoja ili kusudi kuhakikisha Taifa letu sasa linapiga hatua. Kwenye alizeti, niishauri Serikali tuna mifumo kwenye nchi hii mingi sana, mkiingiza bodi na kadhalika tayari lile soko litashuka. Leo mwenzangu wa Singida amezungumzia ni walimaji wazuri sana ni kwa sababu hakuna bodi pale ukiingiza tu bodi lazima patakuwa na tatizo, itaanza kushuka na kadhalika. Tuyaangalie sana hizi bodi wakati mwingine yanaliingiza Taifa kwenye matatizo na migongano isiyokuwa na maana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nianze kwanza kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuweza kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi na wananchi wanaipokea kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naishukuru Wizara ya TAMISEMI kwa kazi kubwa na kwa muda mfupi walioifanya na kuonesha kwa wananchi kwa kuchukua hatua kwa wale wanaofuja fedha za Serikali. Naiomba Wizara hii ijaribu kuangalia maeneo mapya hususan Wilaya ya Itilima, ni Jimbo jipya na Wilaya mpya, takribani miaka 20 liko upinzani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli, wananchi hawa wameweza kufanya kazi kubwa ya kutekeleza Sera za Serikali ya Awamu ya Tano. Serikali ya Awamu ya Tano inasema kila kijiji kuwe na zahanati. Tunavyozungumza hivi, tunazo Zahanati 29 na zahanati nane ziko katika hatua za mwisho. Naiomba Wizara iweze kuleta fedha za kumalizia hizo zahanati ziweze kufanya kazi, ukizingatia Wilaya yetu ya Itilima ni Wilaya ambayo haina Hospitali ya Wilaya. Tunategemea sana hizo zahanati zitapunguza kasi katika maeneo ya Maswa pamoja na Wilaya ya Bariadi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza tu Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa inayoifanya, vilevile na Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya pamoja na wasaidizi wake. Nataka niwaambieni ndugu zangu, Awamu ya Tano imewagusa Watanzania wote na haya tunayoyazungumza na wao wanasikia. Kwa kweli, kazi inayofanywa, kila mtu anaiona na anaitazama. Ni sehemu pekee kwa muda mfupi wameweza kutekeleza majukumu makubwa na ya msingi kwa kuleta mabadiliko makubwa katika awamu hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia suala la madawati, Awamu ya Tano imezungumza kwa mapana sana. Tunaozunguka vijijini unakuta shule moja ina wanafunzi 939, ina madawati 36! Unategemea pale tunatengeneza Taifa la aina gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya Awamu ya Tano kugundua na kutoa maelekezo, bado wenzetu wanaendelea kulalamika, lakini hoja ni nzuri ni kuhakikisha Watanzania, watoto wetu, wanapata maisha bora na elimu iliyo bora. Vilevile itapunguza gharama kwa wazazi wetu kununua mashati pamoja na sketi kwa ajili ya watoto wetu watakapokuwa na madawati bora, natarajia na elimu itakuwa nzuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe ushauri, kwenye 50%, kwenye suala la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji. Wengi wamesema, lakini ikumbukwe, lazima tujenge uwezo katika maeneo yetu ya vijiji. Shilingi milioni 50 tutakapozipeleka bila kuwa na elimu ya kutosha, zile fedha zitapotea na hazitaleta impact yoyote katika maeneo husika. Taasisi moja ipo katika maeneo ya Halmashauri inaitwa Idara ya Maendeleo ya Jamii; wale watu wangefanya kazi ya kutoa elimu kwa wananchi kabla fedha zile hazijafika waweze kujua jinsi ya kuzitumia, kuliko kumpelekea mtu lundo la shilingi milioni 50 katika kijiji kimoja, halafu zile fedha zitapotea na hazitakuwa na hadhi yoyote katika maeneo husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo, zile fedha ni nyingi zinaweza zikasaidia na zikatoa umaskini katika maeneo husika. Maeneo yako katika tabaka mbalimbali. Maeneo mengine kuna Vyama vya Ushirika, kuna ma-godown, maeneo mengine wanalima korosho, pamba na kadhalika. Ile fedha ikitolewa na Tume ya Ushirika ikiboreshwa vizuri, ni imani yangu ile fedha inaweza ikawa mtaji mkubwa katika vijiji husika na ikaleta maendeleo makubwa sana kama wenzangu walivyochangia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, nashukuru sana, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja ili Watanzania waweze kufaidika na hii Awamu ya Tano. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naipongeza Wizara ya Nishati na Madini kwa kazi nzuri wanayoifanya wakiongozwa na Mheshimiwa Profesa Muhongo, Naibu wake, Mheshimiwa Dkt. Medard Kalemani pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na watalaam wake wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara ya Nishati na Madini, katika Jimbo langu la Itilima, Makao Makuu ya Wiliya, REA phase two, haikuweza kuweka umeme katika maeneo ya nyumba za viongozi wa Wilaya ikiwemo nyumba ya Mkurugenzi na nyumba ambayo Viongozi wa Kitaifa hufikia pamoja na kituo cha mafuta kilichojengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naombe Wizara ya Nishati na Madini ione umuhimu kwenye REA phase three iweze kuzambaza umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ya Makao Makuu ya Tarafa ipo miradi ya maji ya Serikali iliyowekezwa inahitaji umeme. Mfano Tarafa ya Kinamweli Kijiji cha Nzezei tunao mradi wa maji ambao uko tayari, unafanya kazi kwa kutumia jenereta ambayo inaleta gharama kubwa kwa wananchi pamoja na kituo cha afya cha Zagayu ambacho kinatoa huduma ya afya katika Vijiji 18 pamoja na Wilaya jirani ya Maswa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Kanadi katika Kijiji cha Migato ni center kubwa ambayo inaweza kuongeza mapato makubwa kwenye nchi yetu pamoja na ajira kwa vijana; inahitaji umeme. Kuna baadhi ya Vijiji ambavyo havina umeme katika Jimbo langu la Itilima kama ifuatavyo:-
Tarafa ya Kinang‟weli, Kijiji cha Nhobola, Sunzara, Kidula, Ngwamnemha, Sawida, Isegwe, Mahembe, Kinang‟weli, Isegwa, Lulung‟ombe, Kabale, Sasago, Mlimani, Kashishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Itilima, Gambasuga, Dasina, Musoma, Ng‟wabagwa, Ng‟wangwita, Ikangalipu, Tagaswa, Nseme, Magazo, Nkololo, Mwalushu, Ng‟wamanhu, Ng‟wagwita, Dasina B, Banamhala, Bugani, Isakang‟wale.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Kanadi ambavyo havina umeme ni kama ifuatavyo; Chimwamiti, Shishasi, Ng‟wakatale, Mtobo, Mwabalah, Pijulu, Nkuyu, Ngailo, Migoto, Simiyu, Lali, Madilana, Mhunze, Ngwabulugu, Ngailo, Lali, Nyatugu, Senani Ng‟waogama, Ng‟wangutugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hoja yetu niliyosema, Mheshimiwa Waziri aweze kutupatia hitaji hilo muhimu kwenye eneo langu la Jimbo la Itilima.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuipongeza Wizara hii ya Maliasili na Utalii kwa kazi nzuri wanayoifanya wakiongozwa na Profesa Jumanne Maghembe pamoja na watalaam wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri na yenye ubora wanayoifanya katika kulinda maliasili ya nchi yetu, ambacho ni kivutio cha utalii ndani na nje ya nchi yetu Tanzania na ndicho kichocheo cha maendeleo ya Taifa letu. Natambua Wizara hii ni ngumu na ina changamoto nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hii itazame vizuri kwenye maeneo ya mipaka ya Hifadhi ya Wanyamapori (game reserves), kwani kumekuwa na malalamiko makubwa kwa Maafisa wa Wanyamapori ikiwa ni pamoja na vitendo vya uovu kwa wananchi kwa kuwatoza faini zisizo kwenye utaratibu wa kawaida wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Maofisa wamekuwa wakiwaswaga ng‟ombe na kuwaingiza ndani ya hifadhi hata kama watakuwa nje ya hifadhi. Nashauri Serikali kupitia Wizara hii iweze kutatua kero hii kubwa inayosumbua wafugaji wengi hapa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri wanayoifanya. Watanzania tunaamini na tunaotoka vijijini, Awamu ya Tano ni awamu ya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika sekta ya uwezeshaji, ukurasa wa 19. Niipongeze Ofisi ya Waziri Mkuu kwa jinsi walivyobainisha kuhakikisha viwanda vinafanikishwa katika nchi yetu hii. Kuna mashirika sita ambayo yameorodheshwa hapa na huu utakuwa muarobaini wenye kuleta ajira kwa vijana wetu nchini Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la viwanda linahitaji malighafi. Nitaenda katika ukurasa wa 21, sekta ya kilimo. Sisi tunaotoka Simiyu na Mkoa wa Shinyanga na Kanda ya Ziwa kwa ujumla ni wakulima wa pamba, alizeti, mahindi na vitu vingine. Katika viwanda hivi ili viweze
kuendelea, naiomba Serikali iweze kutumia kila njia inayowezekana kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa wakati ili hivi viwanda viweze kufanya kazi vizuri kwa muda mrefu na vijana wetu waweze kupata ajira kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na mwenzangu aliyemaliza kuzungumza kwamba Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa sana. Ukienda kwenye Idara ya Maji, target ya mwaka 2015/2016 tulikuwa tumejiwekea malengo ya kukamilisha miradi 1,301 lakini hivi sasa tuna miradi 1,801 na bado miradi 509. Mungu atupe nini Chama cha Mapinduzi kwa mambo mazuri yanayofanyika haya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mradi wa kutoka Ziwa Viktoria ambao utahudumia vijiji takribani 253. Niiombe Serikali iendelee kuharakisha kwa maana ya Mji wa Gangabilili pamoja na Bariadi ambako unatoka Mheshimiwa Mtemi Chenge ili wananchi hao waweze kupata maji safi
na salama kwa sababu, mji wetu unakua kwa kasi na mahitaji ni makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yoyote utakayoyafanya mazuri lazima ukosolewe tu. Serikali ya Awamu ya Tano inafanya mambo makubwa sana, leo hapo Morogoro keshokutwa kuna reli inaenda kuzinduliwa ya kilometa 160 kwa saa moja. Ni maajabu ya nchi hii lakini bado watu tunalalamika. Mungu atupe nini ili tujue Serikali inapiga hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tujifunze Waheshimiwa Wabunge kuishauri Serikali kwa maana ya maendeleo na pale inapokosea tuiambie. Mimi ninakotoka Wilayani kwangu Itilima kuna bwawa lilikuwa limejengwa tangu mwaka 2002, hela zinakwenda na zinapotea. Leo hii Serikali ya Awamu ya Tano bwawa lile limejengwa kwa miezi minne, ni maajabu! Serikali ifanye nini na maji yanaendelea kupatikana katika maeneo haya! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda kwenye shule za sekondari na shule za msingi, ukifika maeneo ya kule utadhani umeingia Chuo Kikuu cha UDOM, wakati ni kijijini. Serikali ya Awamu ya Tano imeungwa mkono na Watanzania wote na tuendelee kutia moyo pale Mheshimiwa Rais anapotoa maelekezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anaungwa mkono na Watanzania. Kulikuwa na tatizo la madawati, amezungumza, wananchi wote wa Tanzania wameitikia na wametengeneza madawati ya kutosha na watoto wetu sasa migongo haiugui. Ni kwa sababu wanapata elimu iliyo safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme. Sisi sote ni mashahidi tunakotoka umeme sasa hivi unamulika mpaka mafisi, hata uchawi utaanza kupungua. Ni kwa sababu ya maendeleo hayahaya katika maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Nawapongeza Wataalamu wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya na TANROAD kwa ufanisi mzuri wa kazi wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie upande wa marine. Hii Taasisi ni kubwa, inazo meli 15 ambazo zinatakiwa zifanye kazi katika maziwa yetu matatu kwa maana ya Ziwa Nyasa, Tanganyika na Victoria. Hizi meli zinaweza zikafanya kazi katika maeneo haya na kupata mapato makubwa ya kuongeza kuwa GDP. Itasaidia kuongeza ufanisi wa maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika lina madeni ya wazabuni karibu shilingi bilioni saba. Pamoja na hayo, wafanyakazi nao hawajalipwa zaidi ya miezi 11. Hii inasababisha kukatisha tamaa watumishi wa Shirika hilo. Ikumbukwe hawa watumishi wanategemewa na familia zao. Fedha iliyotengwa mwaka 2016 kwenye bajeti ya shilingi bilioni 1.4 haijatoka hata moja. Hii inasababisha watumishi kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi.

Pamoja na kuwa wanadai, wafanyakazi wamekuwa na moyo wa kizalendo wa kufufua meli moja inayoenda Ukerewe ambayo imeweza kusaidia wananchi kwa huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, Watumishi hao hawajalipia Bima za Afya tangu mwaka 2014. Wafanyakazi hawapati huduma za afya pamoja na michango ya Mashirika ya Umma; NSSF na PPF.

Mheshimwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani na Shirika hili kubwa lililo na meli 15 ambazo fedha nyingi zimetumika lakini hazifanyi kazi? Kwenye bajeti iliyoisha Serikali ilitenga Bajeti ya shilingi bilioni 50 nayo haijapata hatma za fedha hizo zimefanya kazi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kwa kutenga fedha kilomita 49.7 toka Bariadi kwenda Maswa. Tunashukuru sana kwa kazi hiyo nzuri. Naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi hiyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri mnayofanya kwa kufufua mashirika haya ya Serikali yanayoweza kuifanya nchi kuwa na mapato mengi. Mfano, TRL, ATCL, TTCL na TPA. Marine mkiitunza hakika nchi hii itakuwa inapata mapato mengi. Tunayo meli ya MV Umoja ina uwezo mkubwa wa kubeba behewa zaidi ya 20 kupeleka Uganda moja kwa moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya kwa kutatua changamoto ya maji. Nimpongeze Waziri na watumishi wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iweze kutazama upya upande wa tozo ya mafuta kuweka shilingi 100 ili Watanzania waweze kupata maji kwa kutumia mfuko katika fedha za maji zilizopelekwa hadi Machi kati ya shilingi 181,209,813,609. Utaona asilimia ni 52.7 ambazo ndizo zilizotokana na tozo hiyo, upo umuhimu mkubwa kuhakikisha kuwa pesa hiyo ndiyo inafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyikiti, ninaishukuru Serikali kwa kutupatia pesa kwa ajili ujenzi wa bwawa la Itabi, Wilaya yangu ya Itilima pamoja na kupata pesa za Halmashauri kuingia katika utekelezaji wa visima kumi na kupata shilingi milioni 49 kuweka pump kwenye mabomba pamoja na kupata fedha za mradi wa mabwawa sita ya Mwamapalala, Nhobora, Rugulu Sunzura, Chinamili na Sawinda yote hii ni juhudi ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa mipango yote hiyo iliyoanzishwa kwenye bajeti na kiwango cha pesa kilichopangwa na Serikali ifanye utaratibu mzuri wa upatikanaji wa fedha hiyo katika Wilaya ya Itilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayofanya kuboresha elimu kwa Watanzania. Mimi nizungumzie suala la vitabu kwa mtaala mpya kwa shule za msingi. Baada ya mtaala huu kusambazwa shuleni walimu walipewa mafunzo juu ya mtaala mpya lakini vitabu vinavyofaa kwa mtaala huo vimechelewa kufika. Hii inawapa kazi ngumu sana walimu hasa wa darasa la kwanza mpaka la nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu na Wilaya nzima ya Itilima vitabu hakuna kabisa. Kwa hiyo, tuna mtaala mpya lakini vitabu havipo. Naiomba Serikali iharakishe kuleta vitabu ili walimu waone unafuu wa kufundisha watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri wanayoifanya. Niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri, ni wazee lakini ni vijana kwa sababu wametembelea karibu miradi yote ya nchi yetu ya Tanzania. Niwapongeze watumishi wakiongozwa na Katibu Mkuu kwa kazi nzuri wanayoifanya. Niwapongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Simiyu tumeweza kufanikiwa Mradi wa Ziwa Victoria utakaogharimu Euro milioni 300. Mradi huo utavinufaisha vijiji 253, lakini katika Jimbo langu la Itilima vijiji 64 vitanufaika na mradi huo.

Niiombe Serikali, hususan suala la wakandarasi ambao wanatekeleza miradi katika maeneo yetu iweze kuweka kipaumbele pale certificate Halmashauri zinazopeleka kwenye Wizara, waweze kulipa haraka ili shughuli hizi ziweze kufanyika kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua fedha ni kidogo, lakini fedha hii iliyotengwa inaweza ikafanya kazi, hususan pale ambapo itakapotoka. Pia niiombe Serikali iweze kupokea ushauri na mapendekezo tuliyoyatoa, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Maji kwa kutambua kwamba, fedha hizo zitakazotokana na maji na ndizo hizo sasa zinazoweza kufikisha asilimia 19.8 ya miradi inayoendelea hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niiombe Wizara, pale kwenye suala la upangaji wa bei katika miji ambayo wanakuwa wamekamilisha miradi, katika sheria yetu inachukua siku 45, tumefanya ziara tumekutana na malalamiko mengi kwa wananchi kwamba inachukua muda mrefu na kusababisha kufanya vurugu katika baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, niiombe Serikali pale ambapo wanakuwa wamekamilisha waweze kufanya utaratibu wa haraka zaidi hususan kwenye eneo la EWURA, kutoa bei elekezi ili wananchi katika maeneo hayo waweze kupata maji yenye bei salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuendana na udhibiti wa mapato katika nchi yetu niiombe Serikali iweze kufanya utaratibu wa kufanya kama mfumo wa vocha hasa kwenye miji mikubwa ambayo inaendelea kukua ili tuondokane na suala la maji kuwakatia wananchi. Pale ambapo mwananchi atakapokuwa na bili zake na kadi yake atakuwa anajiongoza kulingana na mapato yake na utumiaji wa maji katika maeneo yake. Tukifanya hivyo tutakuwa tumepunguza lawama na tutakuwa tumeipunguzia Wizara majukumu ya kupambana na suala la ukataji wamaji bila sababu. Maji yake yale atakayokuwa ameyalipia ndiyo yatakayofanyakazi katika nyumba yake na sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Wizara, katika Wilaya yangu ya Itilima nilikuwa na mabwawa 17, lakini mabwawa 6 tayari nimeshapata fedha na shughuli zinaendelea kupitia Mkandarasi DDCA. Niiombe tu Serikali iendelee kujenga uwezo katika Kampuni ya Serikali DDCA ambayo inafanya kazi nzuri na inawaridhisha Watanzania hususan watu wa Itilima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo niendelee kuiomba Serikali katika mji wetu wa Bariadi, kwa maana ya kwako Mheshimiwa Mtemi Chenge, pale Somanda kuna tenki kubwa limejengwa lenye uwezo wa kubeba lita 65,000 pamoja na Sima, mji ule unakua kwa kasi. Niiombe Serikali pia iweze kutilia mkazo eneo lile liweze kupata maji safi na salama, ili wananchi wa Mkoa wa Simiyu waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee tu kuipongeza Wizara, niwapongeze Mawaziri, kazi ni ngumu. Watanzania wote tunahitaji kung’aa, lakini tunawategemea ninyi. Pamoja na kwamba ni wazee, lakini ni vijana ambao mmeaminika katika Taifa hili muweze kufanya kazi ambayo italeta tija katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na wasaidizi wake kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya hasa katika suala zima la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kusimamia suala zima la kilimo hususan pamba, tumbaku na kahawa, lakini kazungumzia pamba. Mheshimiwa Waziri Mkuu kutoka kwenye 120,000 kwa miaka mitatu mfululizo ya nyuma, tumevuka sasa hivi tunatarajia kuvuna 600,000, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali hususan katika suala zima la pembejeo, katika mikakati hii mikubwa tunayoifanya, basi ni vema iende sambamba na pembejeo ili kusudi mazao haya yasiendelee kuathirika kwa kukosa pembejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Waziri Mkuu, mazao haya mengi tumeyapata, lakini wale tunaokaa kandokando na uhifadhi, tunalo janga la tembo. Tembo wamekuwa wakivamia sana katika maeneo hayo na kusababisha maafa makubwa katika jamii. Basi nalo hilo katika suala zima la ulinzi iwe sehemu ya kipaumbele, hususan maeneo ya Itilima, maeneo ya Nyasosi na maeneo ya Mwalali na Nkuyu na Longalombogo, basi viwekwe vituo ili tembo hawa wasiendelee kuja kuharibu mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu kwa vijana, Mheshimiwa Waziri Mkuu Wizara yake inayo dhamana ya elimu. Naomba na kuishauri Serikali, hususan katika vijiji vipya na mikoa mipya na Wilaya mpya zilizoanzishwa, kumekuwa na changamoto ya kutokuwa na shule katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika baadhi ya maeneo wananchi wamekuwa wakijenga madarasa, lakini katika Sheria ya Elimu wanasema lazima tuwe na madarasa sita. Sasa mimi kama mwakilishi wa wananchi, wananchi wananiuliza, hivi tutaanzaje kuwa na majengo sita wakati kuna darasa la kwanza litapita, la pili mpaka la tatu na la nne? Kwa nini tusiwe na manne halafu tuendelee na mwendelezo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, vijana wengi wako kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu, ni vyema Wizara ya Elimu ikashauriwa kuwa na mipango ambayo siyo ya kubana sana ili watoto wetu waweze kupata elimu kama tunavyotarajia katika Awamu hii ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara katika Mkoa wetu wa Simiyu. Aliahidi katika Wilaya yangu ya Itilima, nilikuwa sina jengo la utawala, lakini leo ukiingia Itilima mambo yanakwenda vizuri, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la kuanzisha Wakala wa Barabara (TARURA), mimi nishauri katika sehemu ya TARURA, ni vyema hawa TARURA sasa waweze kushiriki katika vikao vya Halmashauri kusudi wapate mawazo kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao. Tutakapofanya hivyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu tutakuwa na uboreshaji mkubwa na ufanisi mkubwa katika kutekeleza majukumu yao. Siyo kama inavyofanya sasa, inafanya yenyewe, wananchi hawajui kinachoendelea katika maeneo husika, lakini katika suala zima, kazi inakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia suala la juzi alilokuwa anazungumzia kuhusu la wanunuzi wa pamba hususan katika kuanzisha Vyama vya Ushirika. Vyama vya Ushirika mwendelee kuviimarisha ili kusudi wanunuzi hao wasije wakapoteza fedha zao pindi msimu utakapofika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la vijana kuhusu mkopo. Nimeingia Bungeni leo ni mwaka wa tatu. Nimekuwa nikisikiliza humu ndani Waheshimiwa Wabunge tukizungumzia habari ya asilimia 10. Naiomba Wizara itengeneze mfumo wa fedha hizi kuwa na kapu moja ili vijana katika Halmashauri zetu nchi nzima wawe wanakopa kwa pamoja na kurudishwa ili hizi fedha ziwe na mzunguko katika maeneo mbalimbali ya vijana na generation ya vijana wanaokuja. Siyo hivi inavyokwenda, fedha hizi zinakuwa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita, nilikuwa napitia katika Mkoa wa Dar es Salaam. Mkoa wa Dar es Salaam mwaka 2017 umekopesha shilingi bilioni 3.9, lakini collection ni shilingi milioni 400. Utaona sasa kizazi kinachokuja huku nyuma, kitakuta fedha hazipo na hizo fedha zitapotea, lakini tukizisimamia vizuri nina imani kwa usimamizi wenu mahiri Mheshimiwa Waziri Mkuu, akilisimamia hili nina imani fedha zile zitasaidia kizazi kijacho na katika mfumo mzima wa uchumi wa viwanda, vijana wetu wanaweza wakajiajiri na wakafanya kazi kubwa sana katika maeneo yetu husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala zima la afya. Naiomba Serikali ya Awamu ya Tano, miongoni mwa Wilaya 67 na Itilima imo kwa kupata Hospitali ya Wilaya. Ninazo Zahanati 28 zimejengwa ndani ya Serikali ya Awamu ya Tano, chini ya Mheshimiwa Dokta Magufuli na wewe mwenyewe Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba zile Zahanati basi Serikali Kuu wazimalizie kwa maana ya kwamba wananchi wameshajenga mpaka hatua za mwisho, lakini ziko Zahanati tatu ambazo zimeshakamilika. Nyumba ya Mganga na kila kitu. Tunachosubiri tu ni kupeleka Wauguzi na tuna tatizo na suala zima la watumishi. Itilima inahitaji watumishi katika kada ya Afya watumishi 630, tulionao ni 120; lakini tuna wakazi 342,000. Kwa hiyo, utaona adha hii inayowapata wananchi wa Itilima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, alipofanya ziara yake ya kwanza katika Mkoa wetu wa Simiyu mwaka 2016, alipita akaahidi barabara. Leo wakandarasi wako site na wanafanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika ziara yake aliahidi ujenzi wa mabwawa katika Wilaya yangu ya Itilima na kule Mwapalala, sasa bwawa limekamilika na maji yanatoka kwa asilimia mia moja. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya. Kweli anaitendea nchi haki na kiapo alichoapa, kweli Watanzania wote tunaamini kazi anayoifanya ni kubwa na nzuri zaidi. Nchi yetu ilikuwa haina usafiri, leo ina ndege tatu na nyingine zinaendelea kuja. Hiyo ni hatua kubwa ya maendeleo.

Ndugu zangu, Waheshimiwa Wabunge tuendelee kumuunga mkono Rais wetu kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Mwenye macho haambiwi tazama. Naungana na maneno ya Mheshimiwa Azza, amesema 2020 wataisoma. Wataisoma kweli kweli kwa sababu kazi iliyofanywa ni kubwa na inaonekana na Watanzania wote wanaikubali kazi mnayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia mambo mengi ambayo mmeyafanya Serikali ya Awamu ya Tano, lakini kubwa zaidi kuweza kujitegemea sisi wenyewe kuliko kuwa manamba wa kuendelea kukopa katika nchi za nje. Unapokuwa mkopaji hata heshima ya nchi haipo, lakini sasa wameshika adabu yao na ndege juzi ilipoteremka kila mtu nadhani alinyamaza kimya ambaye alikuwa haiombei nchi yetu mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia jioni ya leo. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake na Watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya kwa kuteua Majaji ili kesi zisiwe na mlundikano kwenye Mahakama zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie suala la wafugaji. Wafugaji wetu wameteseka sana hususan wanaoishi maeneo ya kando kando ya hifadhi. Mheshimiwa Rais alipoteua Majaji na Majaji hawa wanafanya kazi nzuri sana na kiapo chao walichoapa watatoa hukumu kulingana na mazingira ya maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Wilaya yangu ya Itilima kuna wafugaji walikuwa wamehukumiwa na mifugo yao ikataifishwa; ng’ombe 339 lakini Mahakama Kuu ikaamuru ng’ombe wale waachiwe na wale watuhumiwa waachiwe, lakini cha ajabu mpaka leo wale ng’ombe hawajaachiwa lakini watuhumiwa walishaachiwa. Sasa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana angetueleza yeye kama msimamizi wa wafugaji, anatusaidiaje wafugaji ambao tunaendelea kuhangaika, lakini kabisa azma ya Serikali Awamu ya Tano ni kuhakikisha inakomboa wanyonge na hususan mambo haya yapo kisheria na Kimahakama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wakati anatoa hotuba yake alisema baada ya mamlaka kumruhusu vibali vya Kimahakama aliweza kuteketeza nyavu, lakini sasa baaadhi ya vyombo vyetu, Mahakama imeamuru ng’ombe warudishwe lakini bado wamezuiliwa na mpaka sasa na ng’ombe wanaendelea kufa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba katika majumuisho yake Mheshimiwa Waziri atusaidie, ni kwa nini mambo haya yanaendelea katika maeneo yetu hususan kwa wakulima na Serikali ya Awamu ya Tano ni ya wanyonge na wakumbuke ng’ombe hawa ni wa wafugaji maskini lakini ndio matajiri wakubwa ambao wanatuwezesha humu ndani sisi sote tukiamka asubuhi tunakunywa supu, tukiamka asubuhi tunataka nyama, maziwa na vitu vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kulisema, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Mbunge aliyemaliza kuzungumza katika suala zima la ng’ombe. Mheshimiwa Waziri anaelewa kabisa kwamba maeneo yetu bado hatujawa na miundombinu mizuri katika minada yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kubwa, mnunuzi amenunua ng’ombe wake watano na tunafahamu kabisa wafugaji wetu au wakulima wetu anaweza akauza mazao yake anaamua kwenda kununua ng’ombe au ametoka machimboni akanunua ng’ombe wake hata 10, 20. Akikutana na wale jamaa, anaambiwa huruhusiwi kuswaga ng’ombe zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii wangetusaidia sana kuweka miundombinu katika maeneo yenu mazuri. Nia ni ya dhati na kazi zao wanazofanya ni nzuri sana, wanalinda rasilimali zetu za nchi lakini namwomba Mheshimiwa Waziri achukue huu ushauri akaufanyie kazi ili kusudi tuondokane na adha hizi ambazo zimejitokeza katika meneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa mipango yake mizuri aliyoilekeza katika ukurasa wa 15 na 12 kuhakikisha Kiwanda cha Nyama cha Shinyanga, kinarudishwa na kinafanya kazi katika maeneo yetu. Hongera sana, hiyo akiifanya litakuwa jambo zuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambasamba na hilo, atusaidie katika eneo liliko Maswa Shishiu ekari 10,240 hazina kazi. Sasa hiyo ni sehemu mojawapo ya kutatua baadhi ya changamoto za wafugaji. Ikiwezekana maeneo haya basi tuwape wafugaji waweze kulifanyia kazi kuliko eneo lipo tangu tupate uhuru lakini halina kazi, yanazidi kupoteza muda. Tukiwapa Watanzania na wafugaji wataweza kutusaidia sana kuongeza kipato cha Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo ameifanya. Amebeba dhamana mpaka ya kuhakikisha analinda rasilimali na mapato ya nchi yaweze kuongezeka. Ushauri wangu ni kwamba wavuvi wamelalamika lakini wanatoa mchango kwa kuunga hoja zake anazozileta, lakini sasa kwenye suala zima la upatikanaji wa vitendea kazi, kiwanda cha Arusha kinaonekana kimezidiwa. Baada ya mwezi mmoja au miwili zile nyavu zinaharibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni jambo jema sana Mheshimiwa Waziri akalichukua na kulifanyia kazi. Kuna Kontena za watu ziko bandarini ambazo tayari zimeshaingia hapa nchini. wangetumia ule utaratibu wa kawaida wakazifanyia uchunguzi, hawa wavuvi wakapatiwa zana hizo wakaendelea kufanya kazi yao kubwa na nzuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka Mheshimiwa Rais alipokuwa akizindua kampeni yake Jangwani, alisema anataka nchi ya viwanda, lakini pia anataka Watanzania wasipate shida. Uzuri Mheshimiwa Waziri amepewa dhamana hii ya kusimamia. Naomba sana pamoja na waatalam waliangalie kwa mapana zaidi ili kusudi wakulima na wafugaji waendelee kufanikiwa katika kutimiza azma ya Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, nampongeza Katibu Mkuu. Tena bahati nzuri Mheshimiwa Waziri amepewa Katibu Mkuu mwanamama na mwanaume. Kwa hiyo, una sehemu kabisa nzuri za kulelewa vizuri na akafanya kazi yake vizuri sana na kuhakikisha Watanzania wanapiga hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba hii. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Fedha pamoja na Watendaji wake, Katibu Mkuu pamoja na washirika wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tunalolizungumzia ni muhimu sana na Bunge kama Watanzania lazima tujue safari ya maendeleo inaenda polepole lakini hadi hapo tulipofikia tuko pazuri sana. Leo tunazunguka katika nchi yetu kwa kutumia taxi kwa sababu ya uboreshaji na ukusanyaji mzuri wa mapato yetu. Niwapongeze watu wa TRA kwa kazi kubwa. Nimpongeze Kamishna wa TRA kwa jambo ambalo amelianzisha la kuzunguka na kukutana na walipa kodi wadogo wadogo, ni jambo ambalo tulikuwa hatujawahi kuliona. Leo walipa kodi wetu hawa wanapata elimu nzuri ya kuweza kulipa kodi na kuweza kukusanya mapato mengi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie tu jambo moja. Katika ukurasa wa 69 wa hotuba yake ameeleza mfumo mzuri kwamba fedha zote za Bodi za Mazao zitakusanywa na Mfuko Mkuu wa Serikali, ni jambo jema, atupe commitment itakayokuwa rafiki na time ya kilimo, kwa sababu jambo hili linaenda kwa muda. Wasiwasi mwingi kwa Wabunge ukisikiliza michango yao ni kwamba fedha hizi zikiingia kwenye kapu lile zitapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuhakikishie fedha hizi zitarudi kwa wakulima on time ili tusije tukaachana na muda kwa sababu ukiangalia kwenye pamba au tumbaku yote yanaenda na muda. Mheshimiwa na Wizara yake waangalie ni jinsi gani watakuwa wanarejesha kwenye Bodi husika kulingana na muda wa mahitaji ili tuondokane na hii tabia ya kulaumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba Mheshimiwa Waziri alizungumzia suala zima la kufuta Kodi ya Ongezeko la Thamani kwa mazao ya mifugo. Katika kupitia kitabu hiki na Bill itakayokuja kusomwa nimeona kipengele cha soya lakini Tanzania kama nchi cha muhimu ni kupunguza tozo kwenye alizeti, pamba, mahindi na karanga, ndiyo tutaongeza bei kwa wakulima wetu kwa sababu soya hapa nchini haizalishwi sanasana iko Malawi, iko sehemu ndogo sana kule Songea na inazalishwa kwa percent ndogo sana. Wafanyabiashara wadogo wadogo wanachukua mashudu ya alizeti na pamba. Utakapoiweka hivyo bei zetu zitaendelea kuwa nzuri lakini tutachochea uzalishaji mkubwa wa mazao ambayo tunayatumia wenyewe. Naomba na hilo nalo Mheshimiwa Waziri alichukue na alifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekaa takribani miezi mitatu, tunaitegemea sana Wizara hii kutukusanyia fedha ili tuzipeleke kwenye maendeleo ya wananchi wetu. Kwa Mkoa wetu wa Simiyu tuna mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Viktoria kuja Mkoa wetu wa Simiyu ikiwepo Bariadi, Itilima, Meatu, Maswa na Busega kwa ujumla. Mheshimiwa Waziri ndiye mwenye jukumu kubwa la kuhakikisha anazungumza na wadau wetu, naomba afanye hivyo ili fedha zipatikane mradi ule uweze kufanya kazi haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mifumo ambayo wameipendekeza ni mizuri sana. Mifumo hii ikisimamiwa vizuri inaweza ikaleta tija na tukaondokana na malalamiko ya kila siku. Mifumo hii ya kielektroniki ambayo wanaileta iko vizuri, lakini ziko changamoto ambazo zinajitokeza kila kukicha, wakati mwingine network zinapotea zaidi ya siku mbili, tatu, kwa hiyo, unaweza ukakuta Serikali inapoteza mapato. Mkiweka misingi na mifumo mizuri inaweza ikatusaidia sana tukawa na jambo ambalo linaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila jambo tunalolianzisha tujaribu kulifanyia analysis za kutosha na tuwe na uvumilivu wa kukubali mambo ambayo yanaenda vizuri. Nashauri Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla waendelee kupokea michango mbalimbali ili kushughulikia changamoto zilizopo kwenye maeneo yetu mbalimbali. Lengo ni moja tumekubaliana lazima tuwe na mfumo rafiki utakaosaidia kuleta tija kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni ushauri na naomba mliangalie. Tunazo halmashauri zaidi ya mia moja, tunakusanya kodi na kukopesha mikopo midogo midogo. Nashauri jambo hili kwa siku zijazo Waziri ajaribu kulitazama ili fedha hizi ziende kwenye kapu na taasisi moja ili kusudi vijana wetu wawe wanaenda kuzikopa na kufuatiliwa kwa utaratibu mzuri, kuliko hivi sasa fedha hizi zimekuwa nyingi lakini ukiangalia marejesho yake hayana tija. Fedha hizi ni nyingi ikiwa zitakusanywa vizuri na kuwekwa kwenye kapu na taasisi moja ya kifedha, zinaweza kutoa mchango mkubwa sana na kuleta uchumi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uliopo sasa mfano, Wilaya ‘X’ Afisa Maendeleo akihama mkopo ule unafifia na kupotea/kufa lakini kama kuna taasisi ya fedha imekabidhiwa fedha hizi inaweza kujiendesha vizuri na tukawa na fedha nyingi. Pia kwa kufanya hivyo hizi kelele tunazopiga kila siku kwamba halmashauri hazitengi fedha zitaisha kwa sababu halmashauri husika kwa makusanyo itakayokusanya asilimia 10 itachukuliwa itapelekwa kwenye chombo ambacho kimepewa mamlaka na aliyepewa mamlaka haya lazima azikopeshe kwa vijana wetu ili kusudi tuweze kutengeneza uchumi mzuri lakini vilevile tuweze kuwajengea uwezo vijana wetu kwa ajili ya kujipatia kipato na kizazi kinachokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Nichukue fursa hii kuwapongeza sana Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri sana wanayoifanya katika kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kutoa pongezi zangu katika Mkoa wetu wa Simiyu hususani Jimbo la Itilima. Serikali ya Awamu ya Tano imeweza kututengea fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya lakini na Hospitali ya Mkoa wa Simiyu. Niwapongeze sana Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, niwapongeze sana Wizara ya Maji kwa kututengea fedha kwa ajili ya ujenzi wa mradi mkubwa wa maji unaotoka Busega kuja Wilayani Bariadi pamoja na Itilima na Meatu kwa ujumla. Shukrani kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi zingine ni katika suala zima la ujenzi wa kiwanda cha vifaa tiba. Kiwanda hiki kinajengwa katika Mkoa wetu wa Simiyu, Dutwa ambako ndiko kwenye Jimbo lako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuwashauri watu wa Serikali; pamoja na kwamba sisi Mkoa wa Simiyu na Shinyanga ni wazalishaji wakubwa wa pamba lakini tunaozalisha pamba nyingi nchini ni Mkoa wetu wa Simiyu. Katika kiwanda hiki cha vifaatiba teknolojia iendane sambamba na viwanda vilivyopo sasa kuliko kuwa na teknolojia ndogo matokeo yake haiwezi ikakidhi mahitaji ya wakulima wa Kanda ya Ziwa. Kwa hiyo, Serikali ilitazame jambo hili kwa mapana zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine, tunavyo viwanda vya nguo lakini ukitazama uzalishaji wake na uhitaji wa zao la pamba haufanani. Asilimia 80 tunasafirisha, asilimia 20 ndiyo inayobaki hapa nchini lakini hata hiyo asilimia 20 inayobaki ukikaa na hawa watu wa viwanda wana changamoto zao. Naiomba Serikali, badala sasa ya kuwa na mipango mingi, sera nzuri na kadhalika ni vyema Serikali ikutane na hawa watu na ichukue changamoto walizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Shinyanga kuna kiwanda cha Serikali ya China kiliwekeza kwa ajili ya kutengeneza nguo lakini leo kiwanda kile kinatengeneza nyuzi, kinapeleka nje halafu ndiyo inarudi malighafi. Kwa hiyo, ni suala kujiuliza kama Serikali kwa nini hawa wawekezaji wetu wanaokuja hapa nchini wanatumia gharama ya kuwekeza viwanda hivi na malighafi iko hapa, kila siku tunasema malighafi tunayo ya kutosha lakini kwa nini iende nje na gharama za uzalishaji zinakuwa kubwa katika maeneo yao, unakuta katika uzalishaji mzima hatupati bei nzuri katika mazao yetu. Jambo hili kama Serikali wakilitazama na kujua changamoto zilizoko naamini kabisa Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Uwekezaji ikikutana na hawa watu wanaweza wakapata majibu mazuri na ni kwa nini mazao yetu hayapandi lakini sasa hivi asilimia kubwa utakutana na changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine; Serikali imekuwa ikiendelea kuweka sera zake nzuri. Tulikuwa na viwanda vya ngozi lakini ngozi wakati ilikuwa ikienda nje kwa maana ya Kenya na sehemu zingine bei zilikuwa kubwa na nzuri sana lakini mkaweka sera ya kwamba viwanda vyetu tuvilinde leo ngozi bei zake ni za kutupa hazieleweki. Kwa hiyo, ni mambo ambayo lazima utafiti wetu ufanyike kwa uhakika zaidi na kufahamu kwa nini tunapoweka hiki bei zinashuka. Katika uwekezaji wetu tunaozungumzia lazima tuangalie mambo muhimu hususani kwenye suala la pamba na viwanda vya ngozi na alizeti. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, utakubaliana nami kwamba asilimia kubwa ya wawekezaji wetu wanatoka nje na wawekezaji wetu hawa wanatarajia kupata wataalam kutoka nje lakini sera zilizopo zinawabana kuwa na wataalam wa kuwafundisha vijana wetu hapa nchini kwa sababu bureaucracy ni kubwa. Kwa hiyo, hilo nalo wakiliangalia tutatoka kwenye asilimia 20 tutakwenda mpaka kwenye asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini duniani kote, Mheshimiwa mama Kilango wiki iliyopita alitoa mchango wake mzuri sana akatoa mfano wa Bangladesh. Ni-declare interest mimi ni mwekezaji na bahati nzuri mwaka 2008 tulikwenda kutembelea Bangladesh, karibu asilimia 70 ya watu wa India wanaishi kwa ajili ya viwanda lakini sisi Tanzania tunavyo viwanda na malighafi kwa nini hatuendelei? Ni swali kwa Serikali kwa nini viwanda hivi haviendelei? Kwa hiyo, lazima wafanye utafiti wa kujua kwa nini viwanda vinavyoanzishwa hapa nchini havi-perform kwa sababu zipi na nini kifanyike? Watuletee tutoe ushauri ambao unawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiko kiwanda pale Arusha, Mheshimiwa Jambo alishafunga tangu mwaka 2007 hakijafanya kazi. Ukimuuliza sababu za msingi anazokutana nazo anasema gharama ni kubwa. Kwa hiyo, Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara wakutane na hawa wadau wawaulize wala siyo kutuma Email au kupiga simu wawaulize kwa nini viwanda vyetu hivi havi-perform na kwa nini bei zake zinakuwa ndogo? Utashangaa bei iliyoko soko la dunia inalingana na mtu anayenunua pamba Shinyanga, Morogoro, Dar es salaam tena la kwake linakuwa chini ukimuuliza anasema gharama ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo moja Waheshimiwa Wabunge wanasema kilo moja ya pamba inazalisha masharti matatu, kilo tatu za pamba ndiyo kilo moja ya mahindi. Kwa hiyo, tunapozungumzia kilo moja ya pamba ina maana ni kilo tatu za mahindi lakini siyo pamba tu hiyo hiyo, kuna malighafi ambayo inatarajiwa kutoka nje ili sasa kuunganisha ili vipatikane hivyo vitu ambavyo vinatajwa mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ni suala la umeme. Tunashukuru Serikali imekuwa na mipango mizuri, sasa mipango hii isiendelee kubaki kwenye makaratasi iteremke kwa wahusika kule ili gharama zipungue ili watu hawa waweze kupata profit kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa, narudia kusema na mwaka jana nilitoa mchango wangu, ukiwasha kiwanda bili yako kama ni ya shilingi milioni 30 au 50 utalipa kwa miezi mitatu mfululizo hata kama umezima kiwanda, kwa hiyo, jambo hili ni la kutazama sana. Siamini wenzangu Mheshimiwa Mawaziri kama walishafanya analysis hizo. Ukiwasha kiwanda leo ukaendesha ndani ya mwezi mmoja utalipa mfululizo miezi mitatu KVA. Mambo kama haya yanatengeneza mazingira watu kuona kwaba uwekezaji hauna faida lakini naamini kabisa kama nchi tunazalisha mazao ya kutosha yote haya tukiyachukua kwa pamoja tunaweza tukafanikiwa na tukapiga hatua kubwa katika suala zima la uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwa mambo mazuri makubwa sana hususani kwa wananchi wangu wa Itilima na Mkoa mzima wa Simiyu mambo yaliyofanyika ni makubwa. Naiomba Serikali sasa iongeze speed katika ujenzi wa kiwanda cha vifaatiba pale Dutwa ili mazao yetu yaendelee kupata bei kubwa na nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango wangu huo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utawala Bora. Nianze kuwapongeza sana Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya wakiongozwa na Waziri na Katibu Mkuu, pamoja na Wataalam wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa ushauri katika sehemu ya Watumishi wanaolipwa mapato ya ndani. Watumishi wanaolipwa mapato ya ndani wanafanya kazi kubwa katika Halmashauri zetu. Ni vyema wangechukuliwa nao sasa walipwe katika Mfuko wa Serikali Kuu ili waondokane na suala la kusubiria fedha za mapato ya ndani. Kazi kubwa wanafanya, ni vyema sasa nao hawa wakaingia katika utumishi kama wengine kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani kubwa sana katika Wizara ya TAMISEMI. Kazi wanayoifanya ni kubwa sana. Ni mfano tosha katika kitabu hiki ukikiangalia kwenye jalada hili, Kituo cha Afya cha Magu na maeneo mengine na kwangu Ikindilo na sehemu nyingine, shilingi milioni 500 nakumbuka katika enzi zilizopita ilikuwa ni suala la kufanya upembuzi yakinifu, hela inaisha; lakini leo fedha hizi zinafanya kazi ya kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata shilingi bilioni 1.5 kwenye Halmashauri zetu 67. Ukizunguka katika maeneo hayo, utakuta zile shilingi bilioni 1.5 ujenzi unakaribia kwisha kwa majengo saba. Niseme tu ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, viongozi wetu kazi kubwa wanazozifanya, tuwatie moyo na tuwatie nguvu. Wanafanya kazi kubwa ya kunusuru maisha ya Watanzania, lakini nao hawalali kwa ajili ya kutufanyia kazi zetu nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu. Serikali ya Awamu ya Tano, pamoja na mengi tunayoyazungumza, lakini kama ni kazi, viongozi wetu wanafanya kazi kubwa sana na nzuri sana. Ni suala la kufika mahali nasi kama viongozi, kama Wawakilishi wa wananchi, tuwatie moyo na pale kuliko na upungufu tuwaongezee maarifa wafanye kazi yao vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haijawahi kutokea, nakumbuka mimi nikiwa kule kijijini, shilingi milioni 50, shilingi milioni 40 ilikuwa darasa moja na haliishi. Leo shilingi milioni 15, madarasa katika kitabu hiki utaona yapo mfano hapa katika Wilaya yangu ya Gangabilili, ni mfano wa kuigwa. Leo tukiingia katika Bunge hili tunaona kama kazi hazifanyiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vituo vya Afya na Zahanati, nashukuru na ninaipongeza Wizara kwa kusajili Vituo vya Afya vinne Ikunguilipu, Mwamwita, Maderana na Ndoleji; na kwa ujumla naiomba Serikali pale itakapokamilika watupatie Wauguzi katika Kada hii ili wananchi waweze kupata huduma katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Waziri ya Mkuu kuna Wabunge walichangia, wanasema Idara ya Maji, haijafanya kazi. Mimi nataka nitoe ushuhuda katika Mkoa wetu wa Simiyu hususan katika Jimbo langu la Itilima. Tangu nchi iumbwe, Makao Makuu ya Lagangabilili tulikuwa hatuna maji. Leo Laganganilili, Nkoma, Kabale, Mwamungesha na Habia yamejengwa machujio ya kuweza kubeba takribani lita 200,000. Kusema ukweli Serikali hii inafanya kazi kubwa na lazima tuipongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilayani kwangu pale Itilima tulikuwa hatuna nyumba ya watumishi, jengo la utawala. Tulipata shilingi bilioni 1.5, leo jengo limekamilika na watu wanaendelea kufanya kazi. Naipongeza sana Wizara imenitengea shilingi milioni 900 kwa ajili kumalizia vitu vingine vilivyopo mle. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kunitengea shilingi milioni 500 kwa ajili ya kumalizia Hospitali ya Wilaya. Nami nimhakikishie mwezi wa Nane au wa Kumi njoo ufungue Hospitali ya Wilaya ianze kuwatumikie wananchi wa Itilima. Haya ndiyo matunda tunayohitaji ya Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba TARURA ituongezee bajeti yake. Wilaya yangu ya Itilima ina mtandao wa barabara wa kilometa 562, fedha iliyotengwa ni kidogo, lakini vilevile yako maeneo korofi ambayo hayawezi yakaendana na bajeti hii. Naomba Ofisi ya TAMISEMI pale ambapo wataalam wetu watakapoleta maandiko, basi watusaidie katika maeneo mawili muhimu sana. Tuna daraja la solo ambalo linaunganika na kwa Mheshimiwa Ndassa na daraja la Mwabuki. Tukiunganishiwa hayo, tutakuwa tumefanya kazi nzuri katika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Wizara ya TAMISEMI imefaa. Zamani walikuwa wanasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi, kumbe na Wazaramo wanaweza. Mnachapa kazi vizuri na kazi inaonekana na mwenye macho haambiwi tazama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Naungana na Waheshimiwa wenzangu wote waliochangia katika Wizara hii. Nataka tu kufahamu, kuna mazao matano ya kimkakati, lakini kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri hapa nimetezama sijaona sehemu yoyote ile. Sasa ndiyo utakuta unapata mkanganyiko wa kujua anayesimamia hiyo biashara ni nani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuelewa mwenye dhamana ya biashara na mikokotoo yote tunayohangaika nayo humu ndani, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana hii anaweza akawa na mchango mkubwa sana kuisaidia Serikali na kujua tumekusanya kiasi gani na changamoto zilizoko kwa wafanyabiashara ni kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunalo zao la Pamba, Kahawa, Tumbaku, Korosho na Mbaazi, lakini Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ambaye ndiye kabeba jukumu la kibiashara na Waziri huyu anatakiwa afanye mazungumzo na wafanyabiashara kujua changamoto zao zote na kuzipeleka Serikalini ili zitatuliwe lakini tumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana. Waziri wa Kilimo ndiye mwenye sera, lakini yule ni mzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na malalamiko mengi, kila Bunge likikutana lazima wazungumze, lakini Waziri mwenye dhamana haonekani katika sekta nzima ya biashara. Kwa hiyo, ningeshauri Mheshimiwa Waziri aje atueleze, majukumu yake ni yapi? Labda ni Waziri wa Viwanda tu pekee bila biashara. Naamini kama ni Waziri wa Viwanda na Biashara anaweza akawa na mchango mkubwa na akasaidia nchi hii. Naye tu kwa uelewa wangu, Waziri wa Fedha anaweza akawa ndiyo Mhasibu wake, lakini yeye ndio anaweza akajua makadirio tunayoyakadiria haya tunaweza tukakusanya kodi zaidi kuliko mtu yeyote mwingine humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri mwenye dhamana hajui biashara zinakwendaje hapa nchini, lakini kuna Wajumbe wenzangu wamezungumza vitu vingi. Kuna mambo yamezungumzwa ya OSHA, sijui WFP na kadhalika, yote haya Mheshimiwa Waziri yanakulenga wewe ili uwasaidie wafanyabiashara. Ili Serikali hii isiwe na malalamiko na wafanyabiashara wewe ni jukumu lako kuhakikisha unasimamia sera nzima ya biashara. Ukifanya hivyo, utakuwa umepunguza dhana nzima ya ulalamikaji katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi kuna Wajumbe wamegusia suala la General Tyre, lakini tunacho pale Kilombero mavuno ya Matairi. Watu wa Kenya (Firestone) wanachukua malighafi yetu, inakwenda Kenya halafu ndiyo tunaletewa matairi.

Mheshimiwa Waziri, ukiangalia tu ni magari mangapi yanayopita kwenye nchi yetu kuzunguka wanapohitaji matairi? Kwa hiyo, ni suala ambalo ukiliangalia linaweza likatusaidia na tukapiga hatua kubwa sana katika dhana nzima ya uwajibishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la TBS, wawekezaji wamekuwa wakifanya analysis za kwanza ana kiwanda chake labda cha Oil Mill linachukua muda mrefu zaidi ya miezi miwili, lakini katika dhana nzima ya uwekezaji inaleta changamoto katika maeneo husika. Ningeshauri Serikali iboreshe mfumo mzima wa TBS ili kusudi wafanyabiashara hao wanaowekeza katika nchi yetu, wanapowapeleka sample yao basi ichukue angalau hata siku 30 au 20 sio kwa mieizi miwili na hiyo miezi miwili inachukua muda mrefu. Wameboresha wakaweka TFDA sehemu ya kwanza na sehemu ya pili. Sasa nashauri watengeneze mfumo mzima wa kusaidia dhana nzima na waweke kikanda, isiwe tu Dar es Salaam peke yake wakiweka kila kanda itatusaidia kuhakikisha kwamba watu wanapiga hatua katika dhana nzima ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia suala la masoko, nimeligusia. Serikali yetu kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi tulisema tutaboresha ushirika na tunavyo vyama vya ushirika na tunavyo vinu vinachombaua pamba katika maeneo mbalimbali. Nimeona kwenye ukurasa waa kitabu cha Mheshimiwa Waziri amezungumzia suala zima la kwamba amerudishiwa viwanda vilivyokuwa 156 na amebaki na vingapi na vingapi. Katika hali nzima ya kuhakikisha ananufaisha na kuboresha ushirika, Mheshimiwa Waziri anaweza akaniambia ni maeneo yapi ambayo ushirika umeimarika na unachakata mwenyewe bila kupitia fedha za wafanyabiashara. Naomba nalo hilo atusaidie katika majumuisho yake kwamba ameboresha hiki na amepiga hatua kufikia mahali hapa itatusaidia nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima lingine, wenzangu wamezungumza mchana hapa, kuna kiwanda cha BORA tena ni cha kizalendo cha Watanzania, Mheshimiwa Waziri atusaidie malalamiko haya watu wanayoyazungumza kulingana na uzalishaji uliopo hapa nchini, taasisi zote za kiserikali ziangalie namna gani ya kwenda kuunga jitihada hizi za wawekezaji walio kwenye maeneo yetu ili wasaidie kuongeza uchumi wa nchi na pato la Taifa, kuliko hivi sasa watu wanazalisha mali inakuwa nyingi, matokeo yake ngozi inakosa mahali pa kununuliwa ni kwa sababu mali haitoki. Mheshimiwa Waziri akitusaidi hilo atakuwa ameweka mfumo mzuri wa kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anao wataalam waliobobea kwenye eneo lake hilo la kibiashara, naamini akiyachukua haya mawazo na akitengeneza mfumo wa kufanya mazungumzo kama Waheshimiwa Mawaziri wengine wanavyofanya, trip ijayo hatutampigia kelele, lakini sasa hivi ni kukutana tu mitaani anakwenda huku na huku, lakini walenga hajakutana nao na wana mawazo mazuri, naamini akishirikiana nao mtu wa kilimo abakize kuzalisha, suala la biashara asimamie Mheshimiwa Waziri itatusaidia na ndio maana miaka ya nyuma Kilimo, Chakula, Ushirika na Masoko ilikuwa ni Wizara moja lakini wakaona watofautishe, sasa leo tunavutana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri katika hili akitufanyie utaratibu huu, biashara zitasonga mbele na shughuli zitakwenda mbele zaidi. Hilo litakuwa sehemu kubwa sana ya kuongeza uchumi katika maeneo yetu na nchi nzima kwa ujumla. Haya akiyachukua Mheshimiwa Waziri itatusaidia sana lakini tutakapokuwa tunaendelea kupiga kelele na Mheshimiwa Waziri wa Biashara anakuwa ni sehemu, leo ameomba bilioni 100, yeye ni sehemu kubwa ya kuwezesha shughuli hizi zisitembee mara moja, kwa sababu wafanyabiashara wote anao mwenyewe, sasa sielewi ni kigugumizi gani ambacho anakipata, anashindwa kukutana nao na kupata mawazo mazuri ya kuhakikisha nchi inapiga hatua na uwekezaji unakwenda kwa kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri asipofanya hivyo itakuwa kila siku watu tunalalamika lakini mwisho wa siku hakuna jibu lolote lile na mwisho wa siku kama walivyosema wenzangu mchana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri wa Kilimo, hotuba nzuri. Nimpongeze Katibu Mkuu pamoja na timu yake ya Wakurugenzi, Wenyeviti wa Bodi zinazoshughulikia mazao yetu. Nitaanza na kutoa pongezi zangu kwa Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyoingilia masuala ya mazao ya biashara, Kahawa, Pamba, Tumbaku nakadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka kutoa ushauri kwa Mheshimiwa Waziri mwaka huu tulikutana na wewe ukasema mambo ya pembejeo ulikuwa na mashaka lakini nafurahi sana katika kitabu chako ukurasa wa 37 jinsi viuatilifu vilivyopatikana katika maeneo yetu, nasema ahsante sana. Naiomba Serikali; mwaka jana tuliazimia katika Bunge kuwa ifikapo tarehe moja Mei kila mwaka lazima msimu wa zao la pamba uwe umefunguliwa ili wananchi waweze kupata fedha katika kipindi hicho. Tulileta hiyo hoja binafsi kwa makusudi kwa kutambua maeneo tunayotoka na wananchi wetu adha wanayoipata; kuanzia mwezi wanne kunakuwa na changamoto ya uhitaji wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anisaidie, kuna baadhi ya maeneo hadi sasa makampuni hayajapata vibali kwa ajili ya kuingia kununua. Lakini ieleweke kwamba sisi kama nchi na kama taifa tunategemea wakubwa wetu walioko nje Duniani kule kwa ajili ya mazao yetu haya. Bila kuwa na mipango na mikakati na utaratibu litakuwa Bunge na itakuwa nchi ya kulalamika kila kukicha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaamini tukisimama vizuri tukashirikiana kwa pamoja Waheshimiwa Wabunge, wenyeviti wa Bodi zile husika, wafanyabiashara, tutatatua changamoto tuliyonayo hii. Haya mengine Mheshimiwa Waziri mnapita katika kipindi kigumu lakini mimi ninaamini tukiweka mazingira ambayo yatakuwa rafiki tutaondokana na zana nzima ya kila mwaka lazima zao la pamba wakae wakutane kupiga kelele, tumbaku wapige kelele, kahawa wapige kelele ilhali waamuzi tuko ndani ya Bunge hili. Kwa hiyo naamini tukisimama kwa pamoja na kuweka utaratibu na tukatumia taaluma za wataalam naamini tutafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshuhudia miaka mitatu katika Bunge lako Tukufu lakini nimeshuhudia katika mikutano ya wadau hakuna jambo lolote la maana tunaloondoka kwa kuzungumza isipokuwa ni kutimiza wajibu tu. Naiomba Serikali kupitia Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, hebu lisimamie hili jambo ukae nalo kwa makini tuondokane na mambo ambayo hayana maana. Kinachotuletea matatizo ni kuchelewesha utekelezaji lakini dhana ni nzuri. Leo ukisoma kuhusu zao la pamba zao linaendelea kuteremka lakini hatujui hatima yake ni nini, tutaanza tena kulalamika lakini majibu tunayo sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge pamoja na wanaojua dhamana ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi ningeomba sana suala hili hasa kwenye pamba; nazungumzia sana kwenye pamba kwa sababu natoka kwenye pamba na nita- declare interest kwamba mimi ni mnunuzi wa pamba, najua changamoto wanazozipata wananchi. Siku mbili hizi pale Kishaku kuna watu wamekamatwa wananunua pamba shilingi 500 kwa kilo. Kwa hiyo utaona ni adha gani wananchi walivyo na shida. Ana mali yake anahitaji hela, hiyo ulichukue na ulifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, nilimsikiliza kwenye hotuba yake kwenye kipindi akielezea habari ya ushirika. Ushirika umeleta tija katika maeneo yetu kuwa na ubora wa pamba ambao ni mzuri na tunahangaika sasa, navyoona kadri tunavyokwenda tunaweza tukaanza kupata premium ambayo ilikuwa imepotea kama senti tatu na kuendelea kwa ubora tunaoendelea nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini changamoto iliyopo lazima ushirika muendelee kuuimarisha si maneno ya kukutana kusema tumekubaliana, hapana; na Mheshimiwa Waziri nikushauri, mwaka jana tuliingia kwenye ushirika na wengine tulikuwa tuna wasiwasi nao lakini tunaanza kuona inakokwenda. Ta hivyo bado kuna vitu vinakuwa vinaongezeka kila mwaka. Ningeshauri Serikali tuwe na mfumo tunaoanza nao wa kwanza tunapata na majibu yake, si leo tukianza mwaka huu baada ya miezi mitatu unasema wakulima wote wafungue account, baada ya miezi miwili tena unakuja na ajenda nyingine; ningeomba kwa jambo hili tuwape muda watu tusiwe tukijiaribia hili tunakuja na jingine inatutia mashakani na tunaleta wasiwasi kwa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ieleweke kwamba benki tulizonazo zina uwezo mdogo kuwafikia wananchi vijijini. Tulikuwa na benki NBC ikabadilishwa kuwa NMB kwa maana ya Rabobank ndio watakuwa washughulikiaji wakati wa kusaidia wakulima wetu; lakini maeneo mbalimbali na wilaya nyingine zilizoko humu ndani hazina benki za hizo NMB. Kwa hiyo utawezaje kupeleka fedha kijijini zaidi ya makampuni labda 10 halafu waingize kwenye account halafu yule mwananchi atoke kilomita 150 kwenda benki; mtaona hata walimu wanapoitapa ile adha ya hela zao kwenye mabenki. Kwa hiyo kutakuwa na changamoto nyingine ambayo sio rafiki kwa wakulima na kutuletea maswali yasiyokuwa na maana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali mifumo hii iendelee kusimamiwa vizuri. Pia tusimamie kupata viongozi wa ushirika wenye weledi na wenye uchungu na watu. Yako malalamiko, baadhi ya wahasibu waliochaguliwa fedha wanazolipwa hazitoshi, mtu hawezi kulipwa shilingi 80,000 na huku anasimamia mamilioni ya watu. Maana yake ni kwamba unakaribisha wizi mwingine kwenye ushirika huo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningeomba hao watu wanaosimamia fedha wapewe angalau posho kubwa ainayoweza kulingana na hadhi yao kama wasimamizi wa fedha za umma au za wafanyabiashara itatusaidia kuliko mtu anashinda njaa analipwa 80,000 mshahara na huku anapokea mamilioni ya fedha; unatengeneza ushawishi moja kwa moja kuibiwa fedha hizo na matokeo yake tunaanza kusema ushirika haufai; kwa hiyo niombe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho nimpongeze Mwenyekiti wa Tume ya Ushirika kaka yangu Titus Mlengea Kamani kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya sasa aendelee zaidi kule chini kuhakikisha anasimamia vizuri.

Mheshimiwa Mwneyekiti, niwapongeza sana Bodi ya Pamba nimpongeze Dkt. Kabisa alistaafu lakini amerudi na pamba sasa imeanza kuongezeka muendelee…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo alitoa Bunge la Kumi na Moja na Bunge la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Spika, kwanza naunga mkono hoja na niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano katika vipindi vyake vyote viwili kwa kazi kubwa na nzuri na jinsi hotuba zake Mheshimiwa Rais alizokuwa akizitoa hapa Bungeni na kwenda kujibu mahitaji ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo nataka kushauri Serikali yetu ya Awamu ya Tano, katika kupitia hotuba ya Mheshimiwa Rais alipokuwa akihutubia Bunge hili tukufu alisema anao mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba anajenga uwezo kwa Watanzania kuwa mabilionea lakini kuhakikisha kuwa wakulima wanaweza kupata mbegu zilizo na tija. Mambo haya yanaenda sambamba pamoja na kuwa na elimu bora lakini na kutoa mafunzo kwa wafanyabiashara na wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumekuwa jinsi Serikali inavyofanya kazi zake vizuri lakini nataka kutoa ushauri wangu sehemu ya uwekezaji. Wazungumzaji wenzangu wamegusia suala zima la umeme, kuna changamoto ya umeme katika maeneo mbalimbali. Namwomba sana Waziri mwenye dhamana ya nishati kuhakikisha maeneo yaliyo na changamoto ya umeme hususan kwa Mkoa wetu wa Simiyu na Mkoa wa Katavi, tumeona jitihada zinazofanywa na Wakuu wa Mikoa kwenye maeneo husika lakini changamoto ni kutokuwa na nishati ya kutosha kwenye maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni Serikali kuhakikisha inapeleka pembejeo kwa wakulima kwa muda muafaka. Tunapozungumzia utajiri kwa Watanzania tunategemea kilimo, yaani kilimo cha pamba, kahawa, tumbaku, mahindi na kadhalika. Yote haya yakitekelezwa, naamini tutaendelea kutengeneza mabilionea wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, asubuhi Mbunge wa Hai kauliza swali la msingi sana na Mheshimiwa Naibu Waziri alizungumzia kwamba ushirika ni hiari kwa wananchi lakini jambo hili limekuwa na sintofahamu. Serikali inasema haiingilii ushirika, ni hiari lakini kuna maeneo mfano ni hivi sasa tunavyoendelea na Bunge hili, baadhi ya maeneo choroko zimeiva ambapo mama anapeleka choroko kilo mbili au tatu lakini kunakuwa na mpango wa stakabadhi ghalani.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia stakabadhi ghalani tuelewe kwamba sisi kama Watanzania hatuna uwezo wa kuhifadhi hicho chakula au kukitumia kwa pamoja, tunategemea nchi za nje kuichukua malighafi hiyo. Hivi sasa bei za choroko ni nzuri sana zinakwenda mpaka 1,500 lakini inaporudi kwenda kwenye stakabadhi ghalani, tunarudisha umaskini kwa vijana wetu ambao wanafanya kazi nzuri ya kusaidia jitihada za maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba jambo hilo liwekwe vizuri kwa sababu kumekuwa na mwingiliano mkubwa sana. Kuna watu wanaitwa AMCOS, kwanza hawana maghala lakini wanasema wewe mfanyabiashara nunua sisi tunaomba utuchangie shilingi 50 kwa ajili ya maendeleo ya ushirika wetu. Ni jambo ambalo kwa kweli lisipoangaliwa linaweza likatuletea changamoto kubwa katika utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo naliona, katika mitaala yetu kwenye elimu zetu za juu, tumekuwa na vijana wengi wanaomaliza vyuo vikuu lakini hawana mahali pa kwenda. Jambo hili ni muhimu sana likatazamwa kuanzia shuleni kuanza kuwajengea uwezo wa kujitegemea vijana wetu. Maana yake ni kwamba, vijana wetu wanapomaliza elimu ya vyuo vikuu changamoto kubwa wakitegemea wataenda kuajiriwa na ajira inapokosekana inabaki ni manung’uniko ndani ya mioyo ya vijana wetu hawa na ile elimu inakuwa haina maana kwa kuipata yule kijana, lakini ina maana akianza kujengewa uwezo akiwa darasani na hususan mwaka wa mwisho, akipewa elimu ya ujasiriamali inaweza ikatusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine niendelee tu kuipongeza Serikali kwa miradi mikubwa ambayo inaendelea kuifanya, lakini niiombe Serikali, imewekeza kwenye hospitali zetu za wilaya, hususan Wilaya yangu ya Itilima, jimbo jipya. Ningeomba sana sasa kupeleka vifaa tiba, vitendea kazi na wataalam kwenye maeneo hayo, ili kusudi sasa haya yote tunayoyazungumza yaendane sambamba na utekelezaji wa hotuba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala zima la barabara zetu hususan kwenye maeneo ya TARURA. Yako maeneo ambayo ni ya kiuchumi katika vijiji vyetu, lakini barabara hizo hazipitiki, lakini na bajeti ya TARURA tunaipitisha pamoja ni kidogo, lakini maamuzi yale yanachukua muda mrefu sana kufanya utekelezaji wa hayo majukumu.

Mheshimiwa Spika, ningeomba sana kwa haya niliyoyazungumza basi Serikali iyachukue na kuyafanyia kazi. Naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza nianze kuwapongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya katika Awamu ya Tano na Awamu hii ya Sita. Serikali ya Awamu ya Tano na Serikali ya Awamu ya Sita tulijikita sana kuhakikisha tunapeleka huduma bora kwa wanachi wetu. Tumejenga vituo vya afya tumejenga zahanati na tumejenga Hospitali za Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ambayo kila Mbunge na kila maswali yanapoulizwa tuna tatizo kubwa la watumishi wa kada ya afya. Ningeishauri Serikali katika kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu ilete bajeti mahsusi kwaajili ya kada ya watumishi hawa ili kusudi fedha nyingi ambazo tunaendelea kuziwekeza kwenye zahanati zetu na kwenye hospitali pamoja na vituo vya afya ili majibu kwa wananchi wetu yaweze kupatikana kulingana na utekelezaji wa kazi tunazoendelea kuzifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo ambalo linakuwa la kusikitisha wakati mwingine Kijiji kimoja kina wakazi 4,000, 2,000 huko Usukumani lakini nesi anakuwepo mmoja kwa siku nzima yule nesi tunampa wakati mgumu wa kutoa huduma kwa wananchi wetu ambao tunakuja kuwakilisha humu. Ningeomba jambo hilo Serikali ilichukue na ilifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Hotuba ya Waziri Mkuu imezungumzia mambo ya Ushirika imezungumzia mambo mengi sana. Tunaotoka kwenye mazao ya kimkakati haya ambayo tunayaona kabisa Serikali ina nia nzuri ya dhati kuhakikisha kwamba inatengeneza ushirika, inatengeneza AMCOS, inatengeneza TMX lakini yako majukumu ambayo TMX anatakiwa ayafanye lakini yako majukumu ambayo watu wa ushirika wanatakiwa wayafanye, lakini yako majukumu mwananchi naye ayatekeleze kulingana na jinsi alivyohangaika kupata hayo mazao yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la TMX ni taasisi ya Serikali lakini inatakiwa kutafuta masoko nje ya nchi lakini kinachotokea kwenye TMX ya hapa kinachofanyika yeye anaondoka anaenda kijijini anaenda kuusimamia ushirika na anaenda kuchukua 1% ya bei inayopatikana jambo hili haliwezekani na jambo hili tunawaumiza wakulima wetu na halina tija yoyote katika Taifa letu hili. Nitatoe mfano kwa miaka ya nyuma kulikuwa na chombo kinaitwa Mamlaka ya Pamba ambacho ilipewa jukumu la kuuza pamba yote ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yaliyotokea Shirika lile lilifilisika na lilileta madhara makubwa na hatima yetu leo ushirika wote ulifilisika kwasababu ya vyombo hivi. Na mfano TMX wameanza tangu mwaka 2018 kwa kasi 2019 tukainga na tatizo la kukosa masoko ya zao la pamba TMX hawa nilidhani wangeonyesha njia yao kubwa kuhakikisha kwamba sasa wanauwezo wa kutafuta masoko na kuuza mazao yetu yale lakini matokeo yake hakuna kilichofanyika na Serikali ilibidi kuingilia kati kuhakikisha kwamba wanatatua changamoto hiyo TMX alikaa pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba sana Serikali ijaribu kuangalia inapoleta mipango mizuri hasa inapokwenda kwa wananchi wetu na tuelewe 70% ya watanzania ni wakulima na wafugaji

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, (Kicheko)

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njalu Silanga naona Jirani yako anataka kukupa taarifa Mheshimiwa Boniventura Kiswaga

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba TMX imejiondoa kwenye jambo lake la kimsingi la kutafuta masoko na kuwa dalali wa wakulima kuwanyonya wakulima badala ya kuwaongezea masoko wakulima. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njalu Silanga unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwasababu ni mojawapo ya waathirika katika wilaya yake ya Magu, ilitokea sana mwaka jana na mwaka huu kwenye zao la choroko pale Maswa ulifanyika mnada wakati korosho inanunuliwa katika bei za kawaida ilikuwa 1500 mpaka 1400. TMX walipokuja kufungua mnada wao waliwauzia wakulima bei ya 1350 kwa hiyo, tayari shilingi 1500 ikawa ni short kwa wakulima wetu hawa na ikatolewa order RAS wa Simiyu akasema halmashauri i-top ile tofauti kwa wakulima jambo ambalo yako mambo mengine inabidi Serikali iyatazame na kuyachunguza hasa Wizara ya Fedha kwasababu TMX wako kwenye Wizara ile wahakikishe kwamba unapoleta mikakati ya kuja kuwasaidia wakulima si mikakati ya kuja kuwanyonga wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba…

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Taarifa

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njalu Silanga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Bashe

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu kumpa taarifa msemaji na Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara ya Kilimo imeshachukua hatua kwenye suala la TMX na haitofanya shughuli za minada katika msimu wa mwaka huu na tunafanya tathmini ya ujumla kwahiyo wasiwe na hofu majaribio yaliyofanyika mwaka jana tumeona matokeo na tumeona athari kwahiyo tumeshafikia maamuzi kwamba ushirika utaendelea kufanya shughuli zake za ushirika na TMX itarudi kwenye core function yake. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Nadhani hiyo inatoa picha namna ambavyo Serikali inasikiliza sana maoni ya Wabunge humu ndani mmefanya jambo jema. Mheshimiwa Njalu Silanga.

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa lakini iwe taarifa ya vitendo maana mwaka huu Bunge la Kwanza tulipokaa humu Waziri Mkuu aliulizwa swali la papo kwa papo akaeleza kwamba ushirika TMX hawataingilia katika mazao haya. Kilichotokea mikoa mingine ilianza kutekeleza walipofika Shinyanga wafanyabiashara gari zao zilizuiliwa na kupigwa mnada.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kauli yake Mheshimiwa Naibu Waziri anayoizungumza iwe kauli ya kulieleza Bunge na iwe kauli ambayo ni mahsusi kwa watanzania. Maana tunachozungumza hapa tumetumwa kuja kuwawakilisha watanzania na tumetumwa kuja kuzungumza changamoto zao ambazo wanazipata na cha ajabu zaidi yako mazao mengine hayahitaji hata kuyaingiza kwenye mifumo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyoamini choroko ni zao la wakinamama ambalo walikuwa wakililima vizuri kwa mahitaji madogo madogo sasa unapobeba kilo 3, kilo 7, kilo 7 kwenda kuziweka kwenye godauni unatengeneza umaskini na manung’uniko kwa wananchi wetu hawa. Jambo hili halikubaliki na kwa sababu Serikali hii ni sikivu ya Chama Cha Mapinduzi ninaamini haya ninayoyazungumza wataenda kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu Serikali katika maeneo ambayo imefanya upembuzi yakinifu katika maeneo yetu mfano kutoka Bariadi kuja mpaka Singida ningeomba jambo hili kwenye bajeti hii basi watengee barabara ile iweze kutengenezwa na watu waweze kusafiri na kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna uwanja wa ndege pale Mwanza kuna njia ya kutokea pale Ilemela by pass ya kuingia kwenda airport ningomba Serikali nalo hili ichukue ilifanyie kazi ili wananchi waondokane na msongamano wa kupita pale Mwanza katikati ambao unakuwa ni msongamano mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo Serikali ningeomba kuendelea kuishauri kwamba mambo mengi mazuri yameendelea kufanywa na Serikali ya Awamu ya Tano na naamini na Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kufanya hivyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu tunahitaji sisi ndege ziendelee kununuliwa kwasababu ndege ndiyo huduma mbadala ya haraka kuleta huduma. Lakini ningeomba sana ipatikane ndege ya kutoka Dodoma kwenda Mwanza kwasababu ni watu wengi wanaotoka Mwanza kuja hapa hata viongozi wa kiserikali hawa wakati mwingine inabidi waende Dar es Salaam ndiyo waende Mwanza jambo ambalo linatupotezea muda. Naiomba Serikali ndege zile tatu zije sisi tuendelee kusafiri kwa ndege, tuendelee kutoa huduma nzuri kwa watanzania ili mambo yaende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya haya machache naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba ya Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kwanza nianze kumshukuru Waziri pamoja na Manaibu wake wawili pamoja na Makatibu Wakuu kwa kazi nzuri ambayo wanayoifanya katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe ushauri katika maeneo ambayo katika hotuba yao wameelezea. Wamezungumza suala la elimu, tuko na maboma mengi sana kwenye halmshauri zetu nchini, ambayo wananchi wamejenga kwenye kwa nguvu zao, lakini Serikali imeendelea ikileta fedha kidogo kidogo na kuanzisha miradi mipya. Ningetoa ushauri kwa sababu ile miradi inasimamiwa na halmashauri, fedha zinazopatikana angalau zingekuwa zinakwenda kumalizia zile nguvu za wananchi ambazo tayari majengo yalishajengwa kwa maana ya zahanati, vyumba vya madarasa, pamoja na maabara ambavyo itatusaidia. Jambo hili litawatia moyo wananchi kwenye maeneo yetu kwamba Serikali sasa inakuja kuunga nguvu ya madarasa, zahanati kwa yale ambayo yamejengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba yake Mheshimiwa Waziri amezungumza ataanzisha sekondari, kwenye wilaya yangu nina kata 22, lakini nina kata mbili ambazo hazina sekondari, lakini kata zile mbili, tayari wananchi wameshajenga, Kata moja ya Nkuyu imejengwa kupitia kusaidiwa na TANAPA, tumejenga madarasa manne na yamekamilika bado hatujapata utawala pamoja na nyumba za Walimu. Ningeomba tu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa sasa kwenye mpango huu watuletee hizo fedha kumalizia haya maeneo mawili ikiwepo Ndobola pamoja na Nkuyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TARURA; kwenye eneo lao la hotuba yao wameelezea vizuri sana kufungua fursa za kiuchumi. Uchumi hauwezi ukaufungua kama wananchi hawafikiwi na huduma ya barabara pamoja na zingine. Ningeiomba Serikali pamoja na kile kidogo kinachopatikana, muundo huu wa TARURA wajaribu kuungalia vizuri. Sasa hivi mamlaka yote yapo mkoani, Afisa aliyeko kwenye halmashauri hiyo, yuko peke yake na wasaidizi wake. Kwa hiyo chochote kinachotolewa na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kinafika tu taarifa, mamlaka yote yatafanyika mkoani na baadaye ndio yatashushwa huko kwenye halmashauri. Hatuwezi kwenda na speed tunayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni muhimu sana, ukizungumza Diwani au Mbunge hawezi kuwa kila wakati anakwenda mkoani kwenda kuuliza, barabara yangu imefikia hatua gani, tender imetangazwa lini, yaani ni changamoto na ukiangalia kwenye hotuba yao wameelezea vizuri kwamba barabara zinazopitika ni asilimia 15. Sasa angalia nchi nzima ina halmashauri 180, ina ukubwa wa eneo gani na mahitaji ni katika maeneo yapi, lakini bado kunakuwa na changamoto hapa. Huwa najiuliza mtu wa TARURA yupo chini ya Ofisi ya Rais na Mkurugenzi yupo chini ya Ofisi ya Rais, kuna nini hapa katikati, haya mahusiano ya watu wawili kati ya Mkurugenzi na Msimamizi wa TARURA wakawa kitu kimoja na wakafanya kazi kwa pamoja. Likifanyika hili litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninayo changamoto kubwa ya madaraja yanaunganisha kati ya wilaya nyingine na Wilaya ya kwangu Itilima. Watu wa Itilima hawawezi kutoka Itilima kwenda Bariadi mvua zikinyesha, kuna daraja linaitwa Bulolambesi. Wangetusaidia TARURA, watutengee bajeti kwa sababu bajeti inayokuja haitoshi kabisa kukidhi mahitaji katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo tumelizungumza sana. Mimi napakana na watu wa Kwimba na Mheshimiwa Marehemu Ndasa tulizungumza Bunge lililopita tukielezea daraja la Sawida na hilo linaunganisha Mkoa wa Mwanza na Wilaya ya Itilima na Wilaya ya Maswa. Ningeomba watutengee kwenye bajeti hii, daraja lile lijengwe. Vile vile tunayo madaraja madogo madogo ambayo yanaunganisha kata na vijiji kwenye maeneo yetu, tunayo changamoto kubwa kwenye Daraja na Nhomango, nadhani wataalam kwenye kumbukumbu zao zipo, Walimu wanaofundisha wanatoka toka kata nyingine kwenda kijiji kile husika. Mvua ikinyesha Walimu hawawezi kwenda kutoa huduma katika Kata ya Nhomango. Nalo ningeomba Serikali iweze kututengea hicho kilichopo, ili maeneo hayo yaweze kupata huduma safi na salama,wananchi wetu waweze kupata huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais, hayati Dkt. John Pombe Magufuli, lakini kuna ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye kampeni alipokuja kuzindua pale makao makuu. Tulimwomba lami, Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu, Makamu Makuu ya Lagangabuli ameshafika, tunamwomba sana angalau Wasukuma pale Lagangabuli wapate lami, wamkumbuke mtani wangu kwa kazi kubwa ambayo atakuwa anaifanya kama alivyosema mwenzangu, ameingia na yeye ni jembe kama jembe lililokuwepo kwenye eneo hilo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika vijiji vyetu, Serikali hii ya Awamu ya Sita naamini kwenye hotuba hii waliyoizungumza, watafanya mambo mengi na makubwa na matarajio ya Watanzania tunahitaji yale ambayo wameweka kwenye hotuba yao yaweze kujibu na yaweze kuleta mabadiliko makubwa sana, hasa kwenye sekta ya afya. Wametutajia fedha nyingi ambazo wamezitenga, naamini kabisa kwa usimamizi mahiri fedha hizi zitafika na zitafanya kazi vizuri sana na sisi kule kama Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Madiwani tuko tayari kutoa msaada na ushirikiano wa hali ya juu ili kusudi azma ya Serikali ya Awamu ya Sita iweze kufikiwa kwa kutimiza malengo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunacho Kituo cha Afya Kabale, kuna daraja na bahati nzuri Naibu Waziri wa Afya ni mwenyeji kwenye maeneo yale. Kile kituo mvua ikinyesha hakifikiki, naomba kutoka Nzanzui kwenda Kabale watuwekee angalau fungu kidogo ili eneo hilo liweze kupitika; Kabale pamoja na Lalang’ombe.

Mheshimiwa Spika, baada ya haya machache, naunga mkono bajeti ya Rais kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba hii muhimu sana ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo. Na kwa maelezo yake mazuri sana tunaanza kupata matumaini sisi wakulima wa pamba na wakulima wa mazao mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia kwenye suala la uzalishaji, uzalishaji wetu unaenda sambamba na masoko, kama mchangiaji mwenzangu alivyozungumza. 2019/2020 soko lilipokuwa zuri tulizalisha tani 348, mwaka 2021 tukashuka tukazalisha tani 122, sasa ndio utaanza kujiuliza kwamba, katika Mpango wa Bajeti ya Serikali wanapopanga mambo ya kiuchumi na Mheshimiwa Waziri ametuelezea vizuri sana kwamba, tunategemea kupata fedha za kigeni, tunategemea kupata ajira kwa vijana wetu, ni vitu vingi vinavyojumishwa kwenye suala la kilimo na kuwa na fedha nyingi kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa nilitaka Serikali watusaidie fedha hizi tunazozitenga kila mwaka kwa ajili ya kilimo, lakini fedha hizi hazifiki kwa muda unaotarajiwa, matokeo yake fedha hizi na taasisi kama bodi hizi na nimpongeze tu Mheshimiwa Waziri Bashe jinsi walivyohangaika kupata fedha kwa ajili ya kusaidia wakulima. Na inasababisha taasisi tunazozipa mamlaka hizi zinakuwa na changamoto kubwa sana kwenye suala la kuhamasisha uzalishaji wa mazao ya kimkakati, hususan zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukisimamia vizuri kwenye kilimo, pamba, alizeti, korosho, hasa mazao mawili hapa, tunakuwa na changamoto ya kulalamika mafuta. Alizeti ikizalishwa kwa wingi na pamba tukizalisha kwa ekari ambazo kwenye takwimu zao wameziorodhesha kilo milioni moja laki tano na hamsini na sita, ukifanya tu wapate kila ekari moja kilo mia nane-mia nane au mia tano-mia tano tutazalisha mwaka mzima. Tutakuwa na mzunguko wa mwaka mzima wa fedha, tutakuwa na mzunguko wa mwaka mzima wa ajira, lakini na train zetu nazozijenga zitasafirisha mzigo kutoka Mwanza kuja Dar-es-Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yote hii Mheshimiwa Waziri wa Kilimo tunakutegemea na Ofisi yako na Bodi zako. Na ikienda mbali tunapozungumzia maafisa ugani hawa wanapoendelea kubaki kwenye halmashauri zetu, ni diwani kwenye halmashauri yangu na wote Wabunge ni madiwani, bila kuwa na mkakati mahususi hawa maafisa ugani tunaowatarajia kuwaajiri wakawajibika moja kwa moja kwenye mabodi yetu na ukawapa mikakati na takwimu, tutapiga hatua na tutafika mbali sana, lakini ngonjera hizi za kuzungumza kila siku hatutafika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala la pili kuhusiana na dawa. Dawa zetu hizi mnazozileta wataalamu wetu watafiti, umeelezea hawa TARI, n.k., hayauwi wadudu. Hadi mkulima ambaye yuko kijijini kule hajui mambo ya utafiti anakwambia nimepulizia, nimechanganya hiki na hiki, lakini yule funza hafi. Matokeo yake tunarudi kwenye uzalishaji wa chini. Lakini yote haya mukiyawekea utaratibu mzuri naamini kabisa tunaweza tukapiga hatua na Taifa letu likaendelea kupata mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mbegu, ningeendelea kuishauri tu Serikali kwamba, tunayo mabwawa ambayo yamechimbwa, tusisubiri sana kila mwaka mpaka msimu wa mvua uanze, lakini huku tuna mabwawa. Bora tuwekeze kwenye mabwawa haya, kwangu jimboni kwangu nina mabwawa karibu manne, Bwawa la Habia, Mwamapalala, Nobola, Sawida na Mwasuguya kule Bariadi, mabwawa makubwa kabisa. Mkiwekeza kwenye suala la mbegu hususan kwenye upande wa pamba na pamba inakamilika kwa miezi minne; ukilima mwezi wa sita mwezi wa kumi na moja unavuna, tayari utakuwa umepata mbegu iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hivi sasa tunakwenda kwenye uzalishaji unaokuwa chini na sababu zinakuwa ni nyingi, unaweza ukakuta mbegu zilishapitwa na wakati. Sisi kule kwenye pamba tuna mbegu UK91 ya mwaka 91, leo tuko mwaka 2021 ni miaka 20, jambo hili wataalamu mnalifahamu, lakini kwa sababu tunakaa hapa kutimiza wajibu tunabaki kusimama hivyo bila kuzisimamia taratibu na kanuni za uzalishaji bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukiendelea kusimamia hivyo viwanda vyetu tunavyovizungumzia tayari tutapata malighafi ya kuviendesha vile viwanda, lakini tumewekeza sana kwenye miundombinu na mengine, lakini ningeshauri sana Serikali kwa ujumla fedha hizi kwenye suala la kilimo zitoke ili ziweze kufanya kazi nzuri zaidi. Ikishindikana Serikali mwaka uliopita ilikuja na sera, tulikuwa na bodi na taasisi zetu mifuko hii ya kuendesha mazao mbalimbali ikazichukua, changamoto ikaanzia hapo tukashuka kwenye uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeomba kama Serikali kama kuna changamoto humo basi, taasisi hizi za wadau ziruhusiwe kulingana na mifumo iliyokuwa ikiendeshwa ili tuondokane na matatizo haya ambayo yunayapata. Kwa sababu, unakuta dawa inaenda mwezi wa tatu, sasa mwezi wa tatu unaenda kupulizia nini? Tayari na Serikali inaingia kwenye madeni ambayo hayalipiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaiomba sana Serikali chini ya Mheshimiwa Waziri na umesema umeunda timu inayoshughulikiwa na Mheshimiwa Bashe, nina imani inaweza ikaleta majibu yakutosha, lakini kubwa zaidi tunalohangaikanalo sisi ni uzalishaji kuwa wenye tija, lakini na masoko yakiwa yenye tija, naamini tunaweza tukazalisha uzalishaji mkubwa tukapata mafuta yakutosha, lakini tukapata ajira za kutosha na tukapata fedha za kigeni za kutosha kwenye maeneo yetu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mzunguko wa kilimo, pale ambapo kilimo kinapokuwa kimezalisha kwa wingi zaidi mzunguko unakuwa ni mkubwa wa fedha kwenye maeneo mbalimbali. Bila kuwa na mzunguko wa kuwasaidia wakulima hatuwezi kupiga hatua hata tufanyaje kwa sababu, hata hizi ndege tunazozinunua watu wanahitaji kupanda, train za mwendo kazi tunazozijenga hizi zinahitaji watu wapande. Nani atapanda hizo train kama watu hawana vyanzo kwenye maeneo yao mbalimbali kwa ajili ya kupata nanilii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee tu kusisitiza kwamba, ninaendelea kuiunga Serikali mkono kwa maana ya Wizara kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya chini ya bodi zetu hizi. Naamini tutafanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Mpango wa Taifa. Nitaanza kuipongeza Wizara kwanza jinsi inavyofanya kazi yake na jinsi inavyorejesha mrejesho kwa wananchi na tunaona matunda yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ambayo Serikali ikiyachukua na kuyafanyia kazi, naamini tutakuwa na pato kubwa la Taifa kwenye nchi yetu. Tunayo Bandari ya Dar-es-Salaam, Bandari ya Dar-es-Saalam imezidiwa na mzigo, lakini tunayo Bandari Kavu ya Kwala, wakichukua Mpango Mahususi wa haraka kwenda kuipunguzia Bandari ya Dar-es-Saalam tukaiboreshe ile Bandari Kavu ya Kwala, naamini pato letu litaongezeka kwa kasi sana kulingana na mizigo mingi inayopita hivi sasa. Nasema hivi kwa sababu mizigo inayopita pale ya transit kwa maana ya DRC-Congo, Zambia, Malawi, Uganda pamoja na Rwanda. Kwa hiyo utaona kwamba Bandari ya Dar es Salaam ime-stuck na meli nyingi ukitazama zimesimama zile ni fedha na ndiyo mipango tunayoijadili hapa. Kwa maana hiyo tukitumia ile Bandari Kavu kwa muda mfupi na kwa haraka zaidi naamini pato letu litaongezeka na mahitaji tutakuwa tunayapata kwa haraka zaidi kulingana na vyanzo tulivyonavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Serikali basi iangalie umuhimu wa kuangalia uwekezaji katika maeneo mbalimbali. Tunayo port ya Kigoma lakini na Ziwa Tanganyika, naamini maeneo haya Serikali ikiyachukua na kuanza kuyafanyia kazi, tutapata mapato ya kutosha. Vilevile uwekezaji wetu na mipango yetu tunayoipanga inategemea na mali tunayoingiza kutoka katika maeneo mbalimbali, lakini tofauti za kibiashara ukiangalia kwa Ruvuma tunayo makaa ya mawe, tukiiboresha Bandari ya Mtwara, ina maana katika uchumi, kibiashara zaidi tutavutia wawekezaji wengi wa kutosha na vilevile Bandari ya Mtwara itabeba mzigo wa kutosha kwa maana makaa ya mawe ukiangalia na changamoto iliyopo sasa hivi tutajikuta pato letu linaongezeka kwa kasi kubwa sana. Pamoja na hayo na mipango tunayoendelea kuifanya, tunayo mipango sasa hivi tunakuja na Bima ya Afya, maana yake nini? Mipango na fedha zote tunazozitafuta hizi, tukiboresha mazingira haya yote tunayoyapanga, Watanzania watatibiwa bure kwa sababu tayari watakuwa na mchango ndani ya Taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile juzi Jumamosi wakati tunapitisha hoja za CAG, tulikuwa tunaangalia mapato na matumizi yasiyo rasmi na vitu vingine. Ushauri tu kwenye Mpango wa Taifa kupitia Waziri wa Fedha, basi angeenda kuangalia namna gani ataelekeza fedha zingine, mfano, kwenye halmashauri zetu tunatoza asilimia moja ya mapato ya ndani ambayo wakulima ndiyo wanayazalisha wao na tunatoa asilimia mia moja. Asilimia arobaini inaenda kwenye maendeleo na asilimia sitini inabaki kwa matumizi ya ndani. Kwa nini asilimia ishirini isitolewe ikaelekezwa kwenye sehemu ya Bima ya Afya kwa wananchi ambao wako kwenye mazingira magumu huko vijijini ambayo ukiitengenezea mpango itasaidia kwa Taifa letu kwa sababu wananchi ndiyo hao hao wanaozalisha na ndiyo hao hao tunaowatoza kodi, kwa nini wasibaki na asilimia arobaini ya matumizi na asilimia ishirini ikaenda kwa wananchi na asilimia ishirini ikaenda kwenye maendeleo ambayo tunayatarajia kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, mipango tunayoiweka hii basi tuweke na mipango ya kudhibiti wizi unaoendelea kwenye nchi yetu hii, kwa sababu bila ya kuwa na mpango wa kudhibiti nako ni sehemu ya tatizo. Ukisikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge, lakini na hali iliyopo kule vijijini kwa wananchi na mabilioni tunayoyataja hapa utaona bado hatujafanya kazi ya kudhibiti fedha. Bado tunafanya kazi ya kukusanya mapato mengi lakini matumizi yake yanaenda nje ya utaratibu. Hii ni hatari na wananchi hawawezi kutuelewa, lakini kwa vile Serikali ipo na inasikia ni vyema sana kila ngazi inayohusika ikahakikisha inadhibiti kile ambacho tunakipata ili kiende kufanya kazi inayotarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo naamini kabisa Taifa letu ni tajiri na lina mipango mizuri na kazi zinazoendelea vizuri kwa sababu tunaendelea kupata fedha kutoka nje lakini na sisi humu ndani tuna fedha, ni vyema sana tukatumia tulichonacho pamoja na za nje zikasaidia Taifa letu lakini kwa mipango tunayoiweka halafu fedha hizo zinaenda nje ya utaratibu, kwa kweli hii ni hatari na wananchi hawawezi kutuelewa. Hivyo, ni vyema sana tukajikita kwenye sehemu ambayo tunaweza tukafanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tukienda sehemu ya uzalishashaji. Wenzangu wamechangia vizuri kwamba tunayo maeneo muhimu sana ambayo nchi kama nchi inaweza ikayagawanya. Watawala wa mwanzo Hayati Mwalimu aligawanya majukumu Mtwara akaweka korosho, Lindi akaweka mbao, Rukwa akaweka kilimo yaani kila maeneo aliweka utaratibu. Sasa ni vizuri mipango tunayoipanga tukaangalia nini kwenye nchi yetu ambacho kinahitajika kwa uharaka zaidi? Eneo fulani tukaliwekea utaratibu, tukaanza kutengeneza uzalishaji. Tukiweka katika mazingira hayo, naamini kabisa tutafanya mambo makubwa na kelele zitakuwa zimepungua, lakini vilevile wananchi wataelewa tunafanya nini kwenye Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi. Pia niwashukuru sana Wizara ya TAMISEMI kwa kiunganishi kizuri wanachokifanya kwa wananchi wetu na kutufanya sisi Wabunge tuendelee kutiza majukumu yetu. Nitoe vile vile pongezi kwanza kwa Serikali ya Awamu ya Sita kwa utekelezaji mzuri ambao unaendelea kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo, nina mambo matatu. La kwanza nianze kuwapongeza sana TARURA kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanayoifanya kwenye maeneo yetu. Tulipiga kelele Bunge lililopita tukiona TARURA hawana uwezo, lakini baada ya kuwapelekea uwezo kila mtu ameona kazi wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kwenye Mkoa wangu wa Simiyu, TARURA tuna maeneo makubwa ambayo yanatoa huduma hiyo, lakini changamoto kubwa ya kwanza ambayo Mheshimiwa Waziri na jopo lake niwaombe sana, hawana usafiri wa kutekeleza majukumu yao kwenye Mkoa wetu wa Simiyu. Meneja wa Mkoa anasubiriana na Mameneja wasaidizi kwenda kutekeleza majukumu na fedha wanazileta kwenye maeneo yetu. Tumeona kwenye Jimbo langu la Itilima wametuunganishia katika vivuko, eneo la Nhamango lipo kwenye mpango, Mnamala Mbugani wameshatoa fedha ujenzi unaendelea, Tagaswa ujenzi unaendelea na maeneo mengine mengi kwenye Jimbo langu ambayo yanaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Spika, ombi langu, unapokuwa Makao Makuu ya Wilaya ya Itilima na bahati nzuri Mheshimiwa Naibu analijua sana eneo la Mkoa wa Simiyu, unapoizungumza Itilima mtu anapotoka Golambesi kwenda Makao Makuu ya Mkoa inabidi azunguke kwenda Makao Makuu ya Wilaya ambayo ni kilomita 110 na kuna Daraja la Nyangokorwa linaungana na Wilaya ya Bariadi, wakitutengea fedha kivuko kile kikatengenezwa, wananchi wetu hawa hawatatumia gharama ya kwenda kilomita 110 kwenda kupata huduma ya kiafya kwa maana Hospitali ya Rufaa pale Nyaumata. Kwa hiyo nikuombe sana mratibu wa TARURA utusaidie katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tunapakana na Wilaya ya Magu na tunapakana na Jimbo la Sumve, kuna kivuko kinaitwa Solo ambako barabara imelimwa mpaka kwenye kivuko ukifika pale kulingana na bajeti tulizonazo ukomo unakuwa ni kidogo. Kwa hiyo wananchi wanaotaka kwenda Mwanza inabidi warudi kilomita 120 na ukitoka tena kilomita 120 kwenda Mwanza kilomita 200 jumla 320, lakini angetokea pale Solo kwenda Mwanza angetumia kilomita 95 akawa ameshafika na kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo ni Mto Gomalong unaunganisha Kata ya Nkulu, Kata ya Mwaswale na Kata ya Laini. Nimwombe sana, maombi haya yamekuwa ya muda mrefu, yachukuliwe yafanyiwe kazi ili wananchi wanaoishi kandokando ya maeneo hayo waweze kupata huduma safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ningeomba sana kwenye mtandao wa barabara kwenye Wilaya yangu ya Itilima ulioingia ni mia tano na thelathini na kitu lakini mpaka sasa tuna mia nane na kitu, kwa hiyo 256 hazipo kabisa kwenye mtandao wa barabara na wananchi, wasamaria wema wamejitolea kufungua barabara. Ningeiomba Serikali, maeneo hayo yaingizwe kwenye mpango ili wananchi waweze kupata huduma inayostahili kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, wanapotufungulia barabara hasa Wabunge tunaotoka vijijini huko, wanaongeza uchumi na wanapunguza kasi ya gharama ya usafiri kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, niwaombe sana, lakini kuna miji inakuwa kwa kasi, nina Mji unaitwa Laini, nina Mji unaitwa Migato, nina Mji unaitwa Luguru na Nyamalapa. Maeneo haya yanahitaji kupanuliwa kwa kuwa na barabara. Sasa kulingana na bajeti ya TARURA inayokuja tungeomba kama kuna uwezekano iongezwe ili wananchi wa Wilaya ya Itilima waweze kuneemeka na Serikali ya Awamu ya Sita. Maeneo haya niliyoyataja yana uchumi mkubwa wa kichochezi kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo niiombe sana Serikali iendelee kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya yetu ni mpya, tuna kilomita moja ya lami ambayo imepangiwa, lakini pamoja na haya tuna eneo ambalo kutoka Makao Makuu kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya na barabara zetu ni za vumbi na kwa sababu tunatengeneza afya, ningeomba TARURA kupitia Ofisi ya Mheshimiwa Waziri atusaidie sana maombi maalum, kwa sababu ni hospitali imejengwa kwa gharama kubwa, sasa huduma ya barabara kwenye hili inapokosekana tayari kunakuwa na changamoto kubwa sana. Tuendelee kuomba watutengee angalau lami kilomita tano kwa kila mwaka, itatusaidia sana kuhakikisha wananchi wa eneo hilo kuelekea Nguno mpaka Nanga itatusaidia sana kuhakikisha kwamba eneo hilo limekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la afya; Wabunge wenzangu wamezungumza humu Serikali inawekeza fedha nyingi sana inawekeza kwenye vituo vya afya, zahanati kwenye hospitali. Sasa ni jambo ambalo ni la kusikitisha, tunaweka miundombinu yenye gharama na kilio chetu kikubwa kila Mbunge anayesimama tunalalamikia mambo ya afya.

Sasa najiuliza tunapozidi kuendelea ku-invest lakini bado tuna changamoto kwenye maeneo haya mengine, mfano kwa Itilima tuna Hospitali ya Wilaya mwaka jana tumetengewa milioni 500 tumelipa MSD lakini fedha hiyo bado hata, zimekuja items tano tu, sasa utajiuliza kwamba ni kitu gani tunachoendelea kukifanya katika maeneo yetu haya. Badala ya kuwa na kipaumbele tunaanza jambo moja tunamaliza tunahamia jambo lingine. Sasa nalo kama Serikali walichukue walifanyie kazi hasa kwenye maeneo hayo muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, ninacho Kituo cha Afya Zagayu, ni cha muda mrefu, kimechakaa na hakina wodi ya wazazi, watoto na akinababa wala hakina maabara. Sasa yote hiyo ni changamoto, ningeomba sana Serikali iangalie sana maeneo hayo muhimu ili iweze kutuunganisha na wananchi waendelee kupata huduma safi ili mambo yaende vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Wizara ya TAMISEMI wanatakiwa walifanyie kazi, sisi hapa tunakuwa tunatenga bajeti. Tunatenga kwenye mifuko yetu ya kilimo, kahawa, tumbaku, pamba na kadhalika, vitu vingi. Hata hivyo, katika hali ya kawaida, tukiangalia yale mazao yetu muhimu tukatengeneza kiwango cha fedha, wananchi wetu tuna mpango wa kuwa na Bima ya Afya, kwenye yale uzalishaji unaozalishwa kila Taasisi, bodi inayozalishwa tukakata percent fulani tukawapelekea wananchi, tukapeleka bima kwa afya bure, kwa maana yake yule mwananchi atakuwa amechangia kutokana na mazao yake aliyoyazalisha, atakuwa anakwenda hospitalini kwa sababu ataamini akifika pale atapata matibabu, atahudumiwa na atatoka yuko salama.

Mheshimiwa Spika, leo tunatenga kwenye tumbaku, tunatenga kwenye pamba, tunatenga kwenye korosho; mazao yote ya kimkakati tunayatengea fedha kwenda kulima. Analima huku mtu mgonjwa baada ya kumtengea fedha hizo zikamsaidia huko mbeleni.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Afya, Wizara hii tunaitegemea sana lakini inalinda uhai wa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nitaanza kuwapongeza sana Wizara kwa kazi kubwa na kasi nzuri inayoendelea hivi sasa kwa upatikanaji wa madawa. Jambo hili linakwenda vizuri lakini yote haya baada ya mabadiliko yaliyojitokeza hivi karibuni naamini Mheshimiwa Waziri kwa uzoefu wake atatusaidia sana Waheshimiwa Wabunge na kuhakikisha huduma za kinamama zinaendelea kupatikana katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba jambo moja, Wizara hii ambayo anaisimamia Mheshimiwa Ummy. Sisi kwenye Wilaya yetu ya Itima tumejenga hospitali ya wilaya lakini tumejenga kituo cha afya. Lakini vilevile kuna bajeti iliyopitishwa mwaka jana kwa ajili ya kuleta vifaa tiba, mpaka hivi sasa ninavyoongea na mkandarasi ni MSD, mpaka hivi sasa kati ya vifaa 51 vimekuja item saba tu. Sasa utaona ni namna gani Serikali inavyozidi kuwekeza katika maeneo haya muhimu lakini bado tunakuwa na changamoto hiyo kubwa ambayo na Serikali tayari inaendelea kuleta fedha nyingi katika maeneo hayo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kupongeza tu, Serikali imeendelea kuongeza majengo katika hospitali yetu ya wilaya lakini na katika vituo vyetu vya afya. Changamoto kubwa ni pale ambapo watumishi hawapo wa kutosha. Wilaya yangu ya Itilima ina takribani wakazi 500,000. Watumishi Idara ya Afya ni 171 tu, sasa tuna vituo vya afya vinne na tuna zahanati 31 na tuna hospitali ya wilaya. Utaona ni adha ipi kubwa ambayo watumishi hawa wachache ambao tunawapata na tunawapa kazi ngumu ya kushindwa kuwahudumia wananchi hawa na matokeo yake mtumishi huyu wa afya anafanya kazi mpaka inazidi uwezo wake na wakati mwingine inafika mahala anajibu tofauti kwa sababu tayari akili yake imeshazidiwa jinsi ya huduma aliyotoa kwa siku hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara husika kuna vijana ambao wamechukuliwa kwenye baadhi ya halmashauri kuendelea kujitolea. Katika nafasi hizi ambazo zimetolewa basi iwe kipaumbele kuhakikisha kwa sababu wapate hiyo ajira angalau itatutia moyo na vijana wengine ambao wapo mitaani wataendelea kushawishika kuendelea kutoa huduma na kusaidia kwenye maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine tuna Kituo chetu cha Afya Zagayu ni cha muda mrefu sana hakina wodi ya wazazi, wodi ya watoto na maabara na kimechakaa sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri basi katika mipango yake akiangalie kile na kubwa zaidi ombi langu kubwa ni kuhakikisha tunaletewa watumishi wa kutosha katika Wilaya yetu ya Itilima na Kituo cha Afya cha Mwanunda ambacho ni kipya kimeshakamilika tunatarajia Juni Mungu akipenda kinaweza kukamilika kikaanza kutoa huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa watumishi tulionao hao wachache haitawezekana. Pongezi nyingi tunaendelea kukupa Mheshimiwa Ummy tunachoamini kwamba na pongezi hizi tunakuamini ni mchapakazi na nimsikilizaji mzuri kwa Wabunge na kwa wananchi na kwa wataalam wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tungeendelea kukuomba pale ambapo kuna umuhimu basi tia nguvu ili shughuli zinazofanywa na Mama yetu Samia Suluhu Hassan ziendelee kutimilika kwa vitendo. Tukifanya hivi wananchi wetu na malalamiko haya ambayo tunayazungumza tutakuwa tumeyapunguza kwa asilimia kubwa sana. Changamoto ya afya ni kubwa, kubwa sana lakini tunahitaji sasa kuendelea angalau ku-balance uwiano wa watumishi wetu katika maeneo husika ili kazi hii ifanyike vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na la mwisho, ombi langu kubwa kwa Mheshimiwa Waziri ninaomba sana watumishi utupatie wa kutosha nakumbuka kwenye program ya Mkapa Foundation ulikuja kutupatia watumishi pale Itilima na ukaahidi kituo cha afya pale Makao Makuu. Naomba Mheshimiwa Waziri kiwe kipaumbele chako kwa sababu ni maneno uliyazungumza wewe na bahati nzuri Mwenyezi Mungu amekurudisha kwenye Wizara hiyohiyo, sasa naomba sana utekelezaji huo ufanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya haya machache naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi. Nimshukuru Mheshimiwa Rais na kumshukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu na Makatibu Wakuu, pamoja na waratibu wa taasisi zote zinazoshiriki kwenye mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kutoa pongezi zangu kwa Mheshimiwa Waziri kwa muda mchache ameleta matumaini makubwa ndani ya Sekta ya Kilimo. Na hii nikwasababu Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake wamekuwa vijana wakizunguka nchi hii kusikiliza kero za wananchi, kero za wakulima na kuhakikisha yakuwa wanakuja kuzifanyia kazi niwapongeze sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninayo machache. Kwanza la kwanza Mheshimwa Waziri tukupongeze sana kwa hatu ya kwanza ambayo umefanya kutoa pembejeo bure kwa wakulima hususani kwenye zao la pamba. Mimi nisipoizungumzia pamba sitapata usingizi kwasababu ndio mkoa mkubwa unaozalisha pamba ya Tanzania hii. Na ndiyo inayowapatia wananchi wangu kipato kikubwa ambacho tunakitegemea na mwaka huu wa fedha ulioisha tulipata tena zao la alizeti. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunakupongeza kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa iliyopo ni suala zima la viuatilifu vinavyopatikana. Kwamba vinakuja ndani ya muda, lakini kulingana na elimu ya watumiaji wetu ile dawa haiui wale wadudu. Sasa, kwa kutokuua kule kunasababisha madhara makubwa sana. Jambo muhimu ambalo umelizungumzia leo kwenye suala zima la utafiti mimi nadhani wadudu waliopo sasa ni tofauti na mazoea tuliyonayo. Mwaka huu tungetarajia kupata takribani tani laki 400, lakini naamini tunaweza tukapata 200 au 300. Madhara makubwa yametokana na viuatilifu ambavyo vimepatikana tukavisambaza vijijini bila kuwa na elimu nzuri kwa watumiaji wa hivyo viwatirifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana, kupitia Bodi ya Pamba usimamizi uongezeke. Wamefanyakazi kubwa sana na zao lilikuwa limepotea lakini tunaona matumaini makubwa sana ambayo sasa yanaweza yakatuletea fedha za kigeni nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye suala la mafuta, kwa sababu unapoizungumzia pamba unazungumza mbegu na unapata na mafuta. Kwa hiyo, naamini kabisa tukiwa madhubuti na tukiwa na usimamizi uliobora imani yangu kubwa kwamba tutapiga hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, leo Mkoa wa Simiyu Kamati ya Siasa ya Mkoa ilikuwepo hapa, imekuja kushuhudia jambo kubwa Mheshimiwa Waziri alilolisema, la kufanya majaribio katika maeneo haya ya ushirika. Mimi sina tatizo na ushirika, ninachokuomba Mheshimiwa Waziri hakikisha unatafuta fedha tuwape washirika wa Mkoa wa Simiyu na mikoa mingine kama Kaku, kama Uchato na kama kule Bukombe ili waingie kwenye soko watengeneze ushindani wa kwenda kufanyabiashara na sekta
binafsi. Ukifanya hivyo utatengeneza ushindani mkubwa na imani kubwa…

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumtaarifu mchangiaji kaka yangu Njalu kwamba wananchi wa Mkoa wa Simiyu wanampongeza sana Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri kwa kukubali mwaka huu kuwa na soko huria la zao letu la pamba kwenye Mkoa wa Simiyu, ambapo inapunguza sasa unyanyasaji ulikuwepo kwenye AMCOS zetu kwa kuwadhulumu fedha zao wakulima. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Njalu unapokea taarifa.

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naye alitakiwa apate muda wa kuchangia, naipokea. Ni kweli jambo hili ni muhimu sana. N aamini Mheshimiwa Bashe kwa kufika mpaka kutoa maamuzi hayo alipoteuliwa kuwa Naibu Waziri mwaka 2019 madudu yaliyokuwepo kwenye Mkoa wetu wa Simiyu na kwa Tanzania kwa ujumla anajua na bosi wake siku moja aliomba kusema ushirika ufutwe. Kwa hiyo, ni jambo ambalo ameliona yeye kwa kulishuhudia nawala hajafuta na wala hatuzungumzi kufuta ushirika tunahitaji ni kuboresha wasiwe wagaragaja kama neno lake alivyokuwa akilitumia wakati akiwa hajawa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuwe na sera ambazo haziwezi kuyumbisha Taasisi za Fedha. Sera zilizo imara zilisimama zitatusaidia sana sisi kama nchi kuhakikisha uzalishaji wa mazao yetu tunayafanya yanapata tija na tunapata fedha nyingi za kigeni kupitia mazao hayo. Kwa hiyo naamini, kwa haya ambayo tunaendelea kuyazungumza na tunaendelea kuishauri Serikali wakiyasimamia vizuri tutakuwa na uzalishaji ulio na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tumeona kuna watu wa makombati walikuwepo hapa, basi yale makombati yaende yakafanye kazi, ikibidi Mheshimiwa Waziri awafungie hata GPS ili tuwe tunawaona wakiwa mashambani kabisa kazi wanazokuwa wanazitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pikipiki nazo ziende vijijini, kuna hatari ya kuja kupasuka matairi tena, zikikaa zinapigwa jua muda mrefu tunakuta zinaharibika. Kwa hiyo, niendelee tu kusema kwamba kazi hii nzuri ambayo Waziri anaifanya, naamini kabisa kwamba tutafanya mazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianzisha Benki ya TADB na Benki ya TIB Commercial Bank, hizi zote zilikuwa na madhumuni yake. Mheshimiwa Waziri ameizungumzia Benki ya TADB, jukumu lake kubwa ni kuhakikisha inasimamia kilimo. Sasa leo tunazungumzia allegation na vitu vingi na vingi. Kwa hiyo ningeomba Wizara husika hii Benki tuiangalie kwenye jicho la pekee ili itoe huduma kwenye jamii hii ambayo tunayoitarajia. Tukifanya hivyo, kwa sababu yenyewe haifanyi biashara kazi yake ni kuhakikisha inavyoelekezwa na Serikali inapeleka kusaidia pembejeo, umwagiliaji na vitu vingine vyote kadha wa kadha ambavyo vinawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitumia fursa hiyo na fedha tunazozitenga kwa Wizara zikienda, aliyokuwa anayasema Mheshimiwa Mwijage asubuhi yatatimilika, nchi hii ni tajiri, ina vitu vingi kila kona kuna uzalishaji wa kutosha. Miaka hii miwili bei za mazao yetu zimeendelea kukua kwa kasi ni kwa sababu uzalishaji tunao na watu wetu wanajituma. Nchi za wenzetu kuchuma ile pamba wanatumia mashine, lakini sisi wakulima wetu wanavuna pamba iliyo nzuri na iliyo bora zaidi, lakini nchi zingine kila kitu ni remote, remote. Kwa hiyo utaona bado tuna nguvu ya kutumia, kwa hiyo kama Taifa tuna jukumu, nguvu hii kuitumia hivi sasa ili kizazi kinachokuja kiweze kufaidika na haya tunayoyatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya machache, naunga mkono hoja na nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Pia nawatakia kila la kheri wenye Wizara, mambo yaendelee vizuri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi kukushukuru kunipa nafasi nami niweze kuchangia na nichukue fursa hii. Pia nichukue fursa hii kuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan. Niwapongeze sana watumishi wa Wizara ya TAMISEMI kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya kuhakikisha mnatimiza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025/2026.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitashauri sehemu ya miradi inayoendelea. Sisi Wabunge tunapokuja kwenye Bunge lako Tukufu tunakuwa na mipango ambayo tumeiandaa kwenye halmashauri zetu. Tumehamasisha wananchi kuhakikisha kwamba tunajenga madarasa, tunajenga zahanati, tunajenga vituo vya afya na tunaambiwa tutakapokamilisha miradi hiyo Serikali kuu itakuja kumalizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo sasa linatupa changamoto, fedha za Serikali kuu zinapokuja badala ya kumalizia zinakuja na maelekezo ya kuja kuanza miradi mipya. Tayari majukumu yetu kama Wabunge yanakuwa yamepotea kwa sababu ile miradi inakuwa ni chakavu, haitekelezeki, lakini vile vile na miradi mipya tunayoianza ndiyo sasa inayokuja na hoja za CAG hapa inakuwa na gharama kubwa badala ya kwamba yale majengo tuliyoyaanzisha na yale majengo yamesimamiwa na halmashauri. Viongozi watendaji wako pale, ma-engineer wako pale, hatua zote za kitaalam zimefanyika, lakini inapokuja fedha kutoka Serikali Kuu inasema tunaanzisha majengo mapya, tunaanzisha zahanati mpya, hii tunaiacha na hizo ramani zinabadilika tena zinakuja ramani zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe TAMISEMI iangalie tathmini ya nchi nzima kwenye maboma yote. Zile fedha zinapokuja ziende zikamalizie maendeleo ya wananchi waliyoyaanzisha. Lazima hatutakaa tufike malengo tunayoyatarajia kwa sababu miradi mingi inatakiwa isimamiwe na wananchi, miradi mingi inaenda kuwahudumia wananchi wanaotoka kwenye maeneo husika. Ni vyema tunapofika mahali miradi tukaona inafaa tukaongeza miradi hiyo ili maendeleo yaende.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano na niombe sana Wizara ya TAMISEMI, kwenye wilaya yangu nimejenga zahanati zaidi ya 32. Zahanati 10 zimeshakamilika, lakini bado mipango midogo midogo ya kumalizia, tumewachangisha wananchi mpaka kuchoka. Sasa niiombe TAMISEMI hizi Zahanati za Dasini, Gambasingu, Nkololo, Mwagimwagi,
Nhobola, Kidula, Muhalale, Golambeshi, Laini na Inalo, zina changamoto chache na hizo changamoto sisi kwenye halmashauri tumejibana tumebakiza fedha kwenye jengo la utawala. Waturuhusu zile fedha ziende zikamalizie ili kusudi wananchi waweze kupata huduma ya afya kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyotuelekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kwenye hizi fedha za BOOST. Niombe, wamefanya kazi nzuri kubwa sana Wizara ya TAMISEMI na wanafanya kazi kubwa kuhakikisha tunapeleka elimu kule vijijini, ni jambo jema. Niombe kwenye yale maboma ambayo yako kwenye mipango mizuri, basi zile fedha waangalie utaratibu wa uwezekano wa kuhakikisha kwamba tunaenda kumalizia miradi mikubwa ambayo italeta impact kubwa kuliko kupeleka shilingi milioni 540, unaenda kujenga shule mpya na kuna shule zingine shikizi zaidi ya shule 30 au 40 kwenye eneo hilo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe tu Wizara wakae kuhakikisha kwamba tunatatua hii changamoto ili wananchi kwenye maeneo yale tuwape morali ya kufanya kazi zile. Vinginevyo tutakuwa tunaelekeza michango yetu, lakini mawazo yetu hayatatekelezeka kwa sababu wanajua hata tukianzisha mradi huu hakuna kitakachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze TARURA. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa na nzuri sana na ndiyo watakaotubeba kwa sababu barabara kila mtu anapita hata kama ni mgeni kutoka nchi ya wapi. Atapita kwenye barabara atasema Tanzania iko safi kwenye barabara. Niwaombe waendelee tu kuongeza nguvu ili kusudi tuendelee kuboresha barabara zetu, madaraja yetu na wilaya zetu zikutane wilaya kwa wilaya. Niombe kwa Mkurugenzi wa TARURA atusaidie sana, kuna maombi ambayo tumepeleka lakini ni ahadi za Mheshimiwa, Viongozi Wakuu waliopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mto Gamaloha ambao unaunganisha Kata ya Nkuyu, Mwaswale na Laini. Niombe sana kwenye mpango wa maendeleo na yenyewe iwepo. Vile vile kuna Mto Sanjo tunakutana na Wilaya ya Meatu, nako niombe sana Wizara ichukue hili jambo iweze kutusaidia wananchi wa kutoka Meatu na kutoka Itilima waweze kuunganika kufanya kazi za maendeleo katika maeneo hayo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mto unaitwa Ntagosa unaungana na Ipililo, wilaya mama katika Mkoa wetu wa Simiyu. Niombe sana Wizara ichukue nafasi hiyo kuhakikisha kwamba inatusaidia kwenye maeneo hayo. Jambo hili likifanikiwa tutakuwa tunafanya kazi kubwa na nzuri zaidi kuhakikisha kwamba tunapeleka maendeleo kwa wananchi wetu. Vile vile tutaendelea kutoa hamasa kwenye maeneo haya kwamba Serikali sasa inafanya kazi yake kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, niombe, tuna miradi mikubwa ya maendeleo yetu ambayo tunaifanya, lakini kubwa zaidi tunaomba kupata watumishi. Serikali watuambie na tulishawahi kusema humu ndani kwamba kama tunajenga hizi zahanati tunajenga shule na yote inalenga maendeleo ya wananchi, kwa nini hatupati watumishi wa kwenda kuhudumia zile kada? Tunaamini sasa hivi wameshatoa nafasi hizi, tuombe, kuna vijana wengi wamemaliza vyuo muda mrefu tangu 2018, 2019, 2020, lakini cha ajabu tunasubiria sasa hivi kitakachokuja kutokea unaweza ukakuta wa 2022 ndiyo anachukuliwa, wa 2016, 2017, 2018 anakuwa hayupo. Wanatupa wakati mgumu kwenye majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiombe Wizara inayohusika ihakikishe kwamba sasa jambo hili la utumishi linatatuliwa la sivyo watueleze Serikali, kwa sababu tunajenga miradi inasimama kwa kukosa wale wahudumu wanaohusika. Watuambie kama uwezekano haupo tujipange sisi kwenye halmashauri zetu tujue jinsi gani ya kutoa huduma kwenye maeneo haya na wakifanya hivyo Mheshimiwa Waziri atakuwa anafanya kazi kubwa na nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kazi ya Wizara ni nzuri wanayoifanya na kule na sisi tunawaunga mkono kwa 100%, kwa sababu tunaamini yale ambayo tumeyaahidi na wao wanatusaidia hawalali usiku na mchana kuhakikisha wanachapa kazi ya kuhakikisha wanawahudumia Watanzania. Sasa tuwaombe wachukue mawazo yetu waende wakayafanyie kazi ili tufike hatma ambayo tunaitarajia na kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyotuelekeza kwamba tutakamalisha yale yote ambayo sisi tumekuwa tukiyafanya ndani ya muda wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho niombe nina miji yangu michache ambayo inakuwa kwa kasi sana. Mji wa Lugulu naomba nitengenezewe barabara za mitaa kwenye maeneo hayo, Mji wa Migato barabara kwenye maeneo ya mitaa, Mji wa Laini na Mji wa Mwamapaa na Suzula yote maeneo haya ni ya kiuchumi. Niombe sana Serikali iyachukue na kuyafanyia kazi na kuendelea kuboresha barabara zilizoko vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hii miradi inayofanyika halmashauri za miji na manispaa, lakini miradi hii haiji kwenye halmashauri zilizoko vijijini. Sasa Serikali ichukue wanapokutana kwenye mipango ya kuratibu wajue wanaporatibu mipango maendeleo yale makubwa watu wanaotoka vijijini ndiyo wanaokwenda mjini kukaa pale kwenye halmashauri na kwenye manispaa. Sasa na kule kijijini ili mazao yatoke vijijini kwenda mjini ni vizuri barabara ziboreshwe. Kwa hiyo kwenye miradi inayokuja ni muhimu sana wakahakikisha wanaangalia mazingira yale ili kusudi jamii inayoishi kwenye halmashauri za vijijini na yenyewe ijitambue kwamba kuna umuhimu wa kukaa kule.

Tunapoirundika kwenye manispaa na kwenye halmashauri za miji, tayari tunanyima haki kwenye halmashauri zilizoko vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi. Nawapongeza Wizara kwa mipango na mikakati mizuri ambayo wanaendelea kuifanya na kuleta matumaini makubwa ndani ya sekta ya viwanda na biashara.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia maeneo machache, la kwanza nitazungumzia viwanda ambavyo Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake amevielezea kwamba ana mpango wa kufufua viwanda vya kimkakati. Nitajikita kwenye viwanda vya pamba ambavyo unatoka Kanda ya Ziwa kule, ndio sehemu kubwa ilikuwa na viwanda vya nyuzi enzi za utawala wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Sasa atakuja kutuambia mikakati hiyo ameiweka kuhakikisha kwamba viwanda hivi vya kuchakata zao la pamba, naamini asilimia 70 ya zao la pamba tuna export asilimia 30 inabaki ndani ya Nchi. Sasa na mpango huu ukifanikiwa utatengeneza uchumi wa Taifa lakini vilevile utaongeza ajira kubwa kwa Watanzania hususan vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye zao la pamba lina vitu vingi ambavyo viko mule ndani. Kuna mbegu ambazo hutengeneza mafuta lakini kuna pamba yenyewe ambayo itatengeneza majora, itatengeneza khanga na vitu vingine. Jambo kubwa hapo ili kulinda masoko yetu ya ndani lakini na kuongeza thamani ya maji tunayozalisha hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, la kwanza; ni vizuri makorido ambayo yanaingiza khanga kwa njia za uchochoro yakadhibitiwa ili kuongeza thamani ya pamba katika Nchi yetu ya Tanzania. Vilevile na kuweka mkakati kwa sababu ameweka kwenye hotuba yake kwamba wanaenda kufufua viwanda. Sasa viwanda unavyovifufua hivi lazima tuweke utaratibu, taasisi zote za umma, magereza, jeshi, MSD na vitu vingine vyote vinavyotumia rasilimali hiyo ya pamba. Naamini kwa mpango huu mkiingiza hiyo component naamini kwamba tunaweza tukafanya vizuri zaidi na kuhakikisha kwamba viwanda vinafanya kazi kwa muda unaotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kwenye viwanda vyetu vya korosho kule Mtwara, tunayochangamoto lakini naamini kwenye mpango wenu Wizara mlivyojipanga mkilisimamia vizuri na tukaja na majibu sahihi ambayo yataleta tija kwa Watanzania naamini jambo hili linaweza likafika mwisho na tunatengeneza historia kwenye nchi yetu tukaondokana na maneno ambayo kila siku tukiamka tunahubiri. Sasa tunahitaji tutoke hapa twende kwenye vitendo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia ni suala la kibiashara. Nchi yetu tangu ipate uhuru ilikuwa na viwanda vya cement vichache, kuanzia uhuru mpaka 2020 tulikuwa na viwanda tisa. 2020 mpaka 2023 leo tuna viwanda 14 na maana yeke ni nini? Maana yake wafanyabiashara wanapoongezeka ndio ushindani unaongezeka kupunguza mahitaji kwa wananchi wetu wa kawaida hususan watu tunaotoka mkioa ya Kanda ya Ziwa na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viwanda vyote viko Dar es Salaam, viko Tanga na maeneo mengine lakini wahitaji wakubwa ni nchi nzima kwa maana ya kanda zote kwenye mikoa ambayo inauhitaji kwenye vitu hivi.

Mheshimiwa Spika, ijulikane kabisa, tunajenga barabara, tunajenga hospitali, tunajenga madarasa na wananchi wanajenga nyumba yote inahitaji cement.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikisikiliza jana mjadala huu wa Tanga Cement, ukiangalia Tanga Cement kibiashara pale na Simba ndio ipo kwenye soko na hii Simba iko kwenye soko na zamani Twiga cement nayo ilikuwa inachechemea pale Dar es Salaam. Watu walikuwa wakitumia magari kwenda kupakia, umebahatika sana unachukua wiki tatu au wiki mbili na Tanga Cement leo ndivyo hivyo hivyo ilivyo. Sasa ninajiuliza kama viwanda vinaongezeka na huyu anataka kuuza mali share yake sijui anamuuzia nani? Na ninyi Serikali kama mna mpango mzuri basi mashirika yenu ya umma yaunganisheni yanunue hiyo hisa asilimia 68 ili ninyi mmiliki kuondokana na sintofahamu iliyoko hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tumefikia viwanda 14, bado tunaanza kulalamika kwamba tuna hofu. Mimi sidhani mtu anayefanya biashara awe na hofu, hofu ya aina gani kwenye shughuli ambayo anajipatia kipato. Kwa hiyo, hili jambo ni vyema sana Serikali mkatueleza kwamba kuna nini humu ndani kimejificha ambacho Wabunge hatukifahamu na jamii haijui. Kwa sababu mambo haya yanayojitokeza haya kweli yanatoa taharuki ambayo hatuielewi elewi lakini mimi naamini pale Tanga kuna kiwanda kingine kinaitwa Mawenzi.

Mheshimiwa Spika, sasa najiuliza au kuongezeka kile na kile kiwanda cha Tanga Cement kiufupi hakizalishi vizuri, kiuhalisia kabisa. Hata sasa ukituma magari kwenda kupakia unachukua zaidi ya wiki tatu mpaka nne, wanasubiria. Sasa huyu mwingine ameingia, sasa hapa sijui kunakaushindani kakibiashara. Sasa hapa mtusaidie ninyi takwimu zenu za kitaalamu, kwamba takwimu za uzalishaji kila kiwanda. Hivi viwanda 14 vinazalishaje na mahitaji yetu kama nchi ni kiasi gani na bado sisi hapa tumepakana na nchi ambazo ni jirani Rwanda na Burundi, naona cement wanachukua kutoka Tanzania inatokea Tanga inaenda kule Uganda na Burundi.

Mheshimiwa Spika, sasa yote haya ni vizuri watu wa Serikali mkitueleza mtatusaidia sana kwamba mkakati wenu ni nini na hiki kinacholalamikia ni kitu gani. Ili kusudi tuwekane vizuri tuweze kufanya kazi hii ambayo imetuweka humu ndani kwenye Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, niwapongeze sana taasisi kwa maana ya BRELA na TIC sasa hivi BRELA pale na TIC pale mtaji wako wa dola milioni 50 unapata incentive maisha yanaendelea. Kwa hiyo, waendelee kuboresha mifumo yao, isiwe ina kwama kwama kwa maana ya kwamba ili tusicheleweshe mambo, watu wanahitaji kuwekeza na Watanzania wanahitaji kufanya kazi nzuri kwa ajili ya maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri kwenye Kiwanda chetu cha Vifaa Tiba Dutwa tusifanye maigizo na kama kweli tuko serious tuna fedha za walipa kodi na huku tuna tatizo la ajira. Tunazitenga hela tunazila zinapotea halafu mradi unasimama. Jambo hili halikubaliki na sio sawa sawa, ilikuwa hakuna sababu yoyote ya kuanzisha mipango mikubwa na shughuli zingine zikawa zinakwama kufanyika, tukiamini kwamba tunakuja kupata mwarobaini, matokeo yake ikaka kimya na tukaanza kusikia sikia, mara kinakwenda Morogoro sijui kinakwenda wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani mipango ya Serikali anayoianzisha mtu yeyote kwenye eneo ambalo linalenga jamii ya wananchi. Basi anayekuja mwingine ni kuendeleza na ndio maana mama akasema kazi iendelee. Sasa kazi iendelee maana yake yale yote yaliyokuwepo yaendelee kutekelezwa. Kiwanda kile ni kikubwa na kikifanyiwa kazi naamini kabisa kitatoa solution ya zao letu la pamba katika Kanda yetu ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara hivi karibuni kule kwetu, pale Maswa kuna kiwanda cha chaki hivi ndio kiwanda cha kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vyema ile fedha inayohitajika kutoka kwa vijana wa Maswa basi iende ili kiwanda kile kianze kufanya kazi. Sasa pale kuna bilioni nane zimesimama halafu mambo haya hatuyatekelezi. Niwaombe sana Mheshimiwa Waziri tuna imani kubwa na wewe ni mchapakazi na una weledi wa kutosha. Ni imani yangu ya kwamba mambo haya yakikamilika naamini kabisa tutakwenda vizuri na hitaji kamili litatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya haya machache naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Kilimo, Wizara ambayo ni tegemeo kubwa kwa Taifa, Wizara ambayo imebeba uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Watendaji, Katibu Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri na matumaini makubwa yaliyosheheni ndani ya hotuba yao kwa kuelezea kwamba ni jinsi gani wanakuja kutatua suala zima la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe tu kwamba kama nchi tunategemea sana mvua lakini katika Hotuba yake Mheshimiwa Waziri alivyoielezea ni kweli inakuja kujibu matatizo ya wakulima wa Tanzania. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa na nzuri zaidi lakini itakumbukwa sana mwaka huu, tumeona mazao mengi sana yakikosa mvua na kukosa wakulima mazao ya kutosha kwa ajili ya nchi yetu. Katika suala zima kwenye hotuba yako jinsi ulivyoelezea kwamba unahakikisha utachimba mabwawa na kuleta zana bora za kilimo, haya tukiyachukua naamini kabisa nchi itakuwa imepiga hatua na tutakuwa hatuna changamoto ya kufukuzana na wakulima wanavyotaka kuuza mali zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala la maafisa ugani. Maafisa ugani wetu sawa tunajua wana changamoto lakini ni watu ambao wakitoka kwenye vyuo wanapelekwa kwenye maeneo ambayo sasa waende hawajui wanaenda kukutana na nani. Ikumbukwe miaka ya zamani kulikuwa na nyumba za maafisa wa kilimo kwenye Utawala wa Hayati Baba wa Taifa alikuwa ni afisa ambaye anaheshimika kwenye maeneo, kwa sababu ndiyo mtu pekee anaweza akabadilisha mazingira ya nchi hii kwa maana ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukuombe Mheshimiwa Waziri na Wizara yako hebu weka mkakati mzuri kwa Maafisa Ugani hawa, tukiwawezesha vizuri najua umeanza hatua nzuri za kwanza umewagawia piki piki na umewafungia vifaa kwa ajili ya kuwa-trace lakini siyo hivyo tu na mazingira wanayofanyia kazi yafanane na elimu waliyoipata. Naamini kabisa tutakuwa na uzalishaji ulio na tija ndani ya nchi kwa sababu tayari ni watu ambao wamesomea utaalamu utakaokidhi kwenye mahitaji ya wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuwapongeza Wizara kwa miradi mizuri mnayobuni kwenye Mradi wa BBT ambao mmeanzisha, ni jambo zuri, lakini tuanze turudi na huku nyuma kwa wakulima walioko vijijini, naamini kabisa hawa wakulima walioko vijijini wakiwezeshwa wanaweza wakafanya kazi kubwa na nzuri zaidi. Maana yake ni kwamba kwa sababu tayari wao wana zana wakonayo tayari, hawa vijana tunaowatengeneza wengi wao wanatoka kwenye vyuo wanakwenda kupewa maeneo, lakini kule kijijini kuna wakulima ambao tayari wao wameshajiajiri miaka na miaka na ndiyo waliotufikisha hapa. Kwa hiyo, ombi langu hebu sasa mawazo ya Wizara tuyahamishe tuwapelekee miundombinu iliyosahihi kwa wakulima wetu walioko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mababu zetu, mama zetu tukiwawezesha na sasa hivi tuna changamoto kubwa. Kila humu ndani kuna kesi za uhifadhi, malisho ya ng’ombe na vitu vingine, kila siku kelele ya namna hiyo. Mheshimiwa Waziri wale wakulima walioko vijijini, ukiwapelekea zana kuwawezesha matrekta mimi naamini tutafanya kazi kubwa ukija kulinganisha na hawa BBT utajikuta umefanya kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanapata fursa nzuri katika mnyororo mzima wa thamani ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine sambamba na hayo, tunakaa hapa kama Bunge la Bajeti tunazungumzia mapato. Mapato yanatokana na nini? Mheshimiwa Waziri ameyataja lakini tumpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuwaamini nyie vijana kwa kazi kubwa Mheshimiwa Waziri kwa kuwapa fedha nyingi shilingi bilioni 970. Kwa hiyo tuna imani na ninyi kwamba mnaweza mkafanya vizuri zaidi, kwa umri wenu huo msipotenda mema hamtaenda Mbinguni kwa sababu naamini Watanzania wote wanawategemeeni sana ninyi. Tukisimamia kilimo, mifugo, nyuki na uvuvi naamini kabisa tunaweza tukapiga hatua na nchi yetu ikawa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye sera zetu za kilimo. Mheshimiwa Waziri umetaja unakuja kufanya mabadiliko makubwa kwenye ushirika na kwenye sera nzima ya kilimo. Hilo ndiyo jambo la muhimu maana matamko yanayotokea kila mwaka yanachanganya na kufedhehesha kilimo cha mazao. Mfano tunaotoka Kanda ya Ziwa, ukichukua takwimu za miaka mitatu ya nyuma na mpaka leo tulifika mpaka milioni 350, leo tunazungumzia milioni 170, kwa hiyo tumepoteza kiase gani cha fedha za kigeni tungeingiza kwenye nchi lakini kwa sababu ya kutokuwa na sera iliyobora na iliyo imara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri kwa mipango yako mizuri hii ya kusimamia ushirika pamoja na kilimo ni jambo jema, lakini lazima kwenye ushirika muende mkafanye mabadiliko makubwa kwa sababu mtu mzuri akifanya miaka mitatu lazima atoke. Sasa siamini kama mfumo huu unaweza ukatengeneza mazingira unayoyafikiria wewe, lakini tukiyaacha yakawa open kwamba kiongozi aliyeaminiwa na ushirika au na jamii kwenye eneo husika atatolewa kulingana na changamoto zake lakini kwenye mpango huu wa kuchukua miaka mitatu akishamaliza anaondoka tutapiga kelele kila kukicha hautabadilisha mfumo mzima wa ushirika, kwa sababu ni sehemu ambayo wanaamini wasipomsikiliza boss fulani mambo hayataenda kama inavyotarajiwa. Kwa hiyo niombe sana Wizara haya mambo iyachukue na iyafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)