Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Elias John Kwandikwa (38 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti,naipongeza Serikali kuja na Mpango wa Pili mzuri wa Maendeleo, ambao utagusa maeneo mengi, ikiwemo Ilani ya uchaguzi tulioinadi mwaka jana 2015. Pia napongeza Hotuba ya Waziri Mkuu ambayo inaonesha commitment ya Serikali kwa wananchi wake. Hatua hii na hatua nyingine mbalimbali ambazo Serikali imeendelea kuchukua, imesaidia kuwapa Watanzania mtazamo mpya wa kufanya mabadiliko kuanzia kwenye ngazi ya familia.
Mheshimiwa Mwenyekiti,rasilimali watu, naomba na kuishauri Serikali iangalie kuboresha maslahi ya watumishi ili waweze kushiriki kikamilifu katika kuchangia ukuaji wa uchumi. Na-declare interest mimi ni mhasibu, mkulima na mfanyabiashara pia.
Naishauri Serikali iwatazame kwa jicho kuu watumishi wa Idara ya Takwimu, kwani ikiboreshewa vifaa na huduma wataisaidia Serikali kupata taarifa muhimu zinazohusu hali ya uchumi, changamoto, pamoja na namna ya ufafanuzi wa changamoto kwa wakati. Pia kada ya uhasibu itazamwe, itumike kuisaidia Serikali, kada hii inatumika zaidi kwa sasa kuandaa taarifa tu na hawatumiki kwenye maamuzi, kwani hawaonekani kama viongozi kwenye idara na agency za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti,huduma za jamii katika Jimbo la Ushetu; maeneo ya Majimbo, Halmashauri za Wilaya zilizopo nje ya Makao Makuu ya Wilaya zimesahaulika na Serikali kuendelea kuamini huduma zikifika Makao Makuu ya Wilaya mwonekano unakuwa huduma imewafikia wananchi wengi, hivyo naomba yafuatayo Ofisi ya Waziri Mkuu iyazingatie:-
(a) Kwanza, afya, tunahitaji tupatiwe hospitali ya Wilaya katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu, katika Kituo cha Afya cha Mbika, Kata ya Ushetu. Kituo hiki hivi sasa kinahudumia Jimbo la Ushetu na Majimbo jirani ya Ulyankulu na Urambo. Hospitali ya Wilaya ya Kahama pekee imezidiwa kwani inahudumia Wilaya za Mbogwe, Bukombe, yaani wagonjwa wa nje na ndani ni 600 kwa siku.
(b) Huduma ya utawala; tunaomba kupewa Wilaya ya Ushetu ili usimamizi na uratibu wa shughuli za huduma na maendeleo zisimamiwe vizuri. Tuliahidiwa kupewa Wilaya baada ya kupewa Halmashauri ya Wilaya na Jimbo, jambo ambalo limekamilika (rejea hotuba wa Waziri Mkuu ya 2010/2011).
(c) Ujenzi wa barabara kutoka Mpanda- Ulyankulu- Ushetu - Kahama kwa kiwango cha lami; kama ilivyo kwenye Mpango wa Maendeleo na Ilani ya Uchaguzi, barabara hii itajengwa. Hata hivyo, inaonesha usimamizi wa barabara hii itakayohusu mikoa mitatu, yaani Katavi, Tabora na Shinyanga, inaonesha usimamizi unasimamiwa na Meneja TANROAD Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti,nashauri ifuatavyo:-
(i) Usimamizi ufanywe na mameneja wote, kila mmoja eneo la mkoa wake na kuwe na project tatu ili usimamizi na uwajibikaji upimwe kimkoa.
(ii) Ujenzi uanze kwenye kila Mkoa husika ili huduma kwa wananchi iende kwa uwiano.
(d) Ushirika; suala la ushirika litazamwe, tuwe na ushirika kwenye sekta zote, wafugaji hawana ushirika madhubuti, hivyo wasaidiwe kikamilifu.
(e) Maji; maji yaliyotoka Ziwa Victoria yamefikishwa Wilayani Kahama, kwa nini yasisambazwe kwa wananchi wa Jimbo la Ushetu.
Mwisho, naunga mkono hoja. Taarifa yangu iingizwe kwenye Kumbukumbu Rasmi za Bunge.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shida kubwa sana ya malisho ya mifugo yetu Jimbo la Ushetu kwenye Kata za Ulowa, Ubagwe, Ulewe, Nyankende na Idahina na Mheshimiwa Waziri atakumbuka tumepewa muda wa ukomo 15 Juni, 2016 tuwe na eneo mahsusi la malisho kutokana na kauli ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili ya tarehe 2 Aprili, 2016. Nimesoma hotuba na jedwali Na.12 sijaona kuwa tumetengewa maeneo ya malisho. Naomba ufafanuzi hali ni mbaya na tuna eneo la misitu ya Usumbwa na pori la Ushetu – Ubagwe ambalo linaweza kutuondolea adha na mgogoro wa wafugaji na wakulima wa Jimbo la Ushetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya yana ukubwa ufuatao, Usumbwa kilomita 360 na Ushetu – Ubagwe kilomita 310. Idadi ya ng‟ombe peke yake Jimbo la Ushetu inakadiriwa kuwa zaidi ya 300,000. Hivyo, naomba ulitolee commitment jambo hili na itapendeza pia ukitoa kauli juu ya maeneo yote yanayozunguka hifadhi ya Kigosi – Muyowosi. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara hii kupigania ongezeko la bajeti, pia irekebishe sura yake ya bajeti. Haya ni maoni yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti yetu bado ni ndogo sana, shilingi trilioni 1.4; ni vema tufuate azimio la Abuja (E.F.A Goals). Bajeti ya Elimu ifike ifike 6% ya Tanzania GDP. Mfano, bajeti ya mwaka 2014, GDP ilikuwa inakadiriwa kuwa trilioni 100+, hivyo bajeti ya elimu ingekuwa shilingi trilioni 6.055.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Bajeti ya Elimu kwa matumizi ya kawaida, kujumuisha mikopo ya wanafunzi, nashauri siyo vema bajeti ya maendeleo kujumuisha mikopo ya wanafunzi; hii ina-mislead budget structure ya Wizara. Mbona ununuzi wa magari inawekwa kwenye matumizi ya kawaida?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Idara Ukaguzi wa Elimu itengewe bajeti ya kutosha na iongezewe rasilimali za kutosha ikiwemo rasilimali watu. Kwa sasa mawanda ya ukaguzi ni madogo, yaani asilimia 20 tu. Ni vema ukaguzi uweze kufikia angalau asilimia 30, itasaidia kugundua mapungufu na kufanya marekebisho mapema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara hii ifanyie kazi tafiti zilizofanyika pamoja na ripoti za CAG hususan maeneo ya value for money, audit (VFM Audit). Mfano, wanafunzi kutofanya vizuri masomo ya hisabati, viwango vya ufaulu kwa watoto wa kike na kadhalika, Wizara ifuatilie maoni hayo ili tufanye vizuri na kuinua viwango vya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atusaidie kuanzisha Shule za High School katika Jimbo la Ushetu hususan Shule za Bulungwa Secondary School (Kata ya Bulungwa) na Mweli Secondary School (Kata ya Ushetu). Mimi Mbunge na wananchi tutahamasishana kuongeza madarasa na mabweni, naomba Wizara mtuunge mkono. Naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Spika, kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Waziri wa Fedha. Hotuba ambayo ni muhimu sana; na nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuipongeza Wizara na Watendaji wote, na wote waliohusika kutuandalia kwanza Mpango ule wa Maendeleo kama tulivyousikia; lakini pia hotuba hii nzuri. Niipongeze kwa dhati kwa sababu ukiangalia bajeti hii utaona imezingatia mambo muhimu sana, imezingatia pia mwelekeo ambao tunautarajia. Ukiisoma bajeti hii utaona yako maeneo muhimu sana. Uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, imezingatia maboresho ya mfumo wa kodi na tozo na mabadiliko makubwa sana na sura ya bajeti na mambo mengi ambayo tumeyaona. Kwa hiyo, nipongeze kwa dhati juu ya kuwa na bajeti nzuri namna hii, inatupa matumaini kwamba kweli tunaelekea kwenye uchumi wa kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba mwaka huu ni mwaka wa kizio (it‟s base year) kwa hiyo upo umuhimu wa kuangalia data na kumbukumbu zetu za mwaka huu kwa ajili ya kuweza kuzitumia siku za usoni; ili kuona mwelekeo wa ukuaji wa uchumi unavyokuwa kuanzia mwaka huu. Ni mwaka ambao tumekuwa na Rais mpya, mchapakazi na ambaye anadhamira ya dhati kutupeleka sehemu nzuri, lakini ni mwaka ambao pia tuna Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano mpya na yamkini pia tuna Waziri wa Fedha ambaye kama anavyoonesha kwamba atatusaidia sana ili tuweze kuona hali ya uchumi inakwenda kule tunakostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuwa na mimi nichangie tu upande huu wa data zetu nikizingatia kwamba Ofisi ya Takwimu inafanya kazi nzuri. Nilikuwa nafikiri ni muhimu niseme kidogo hapa, kwamba hii Idara inafanya vyema. Lakini nilikuwa nafikiria nishauri idara hii sasa iwezeshwe kwa haraka ili tuweze kupata data ambazo zitatusaidia kufanya analysis zaidi tunapo kwenda mbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu utaona kwenye kitabu hiki cha hali ya uchumi ile price index iliyotumika ni ya mwaka 2007, inaonesha pale nyuma ilikuwa ina shida kidogo ya uwezeshaji, lakini nilikuwa nafikiria kwa sababu tumeanza mwaka na mambo mapya ni vizuri sasa; hao wenzetu wa takwimu wawezeshwe mwaka huu ili basi tupate price index mpya ambayo itatufanya tuweze ku-determine ukuaji wa uchumi unavyokwenda kwenye hii miaka kumi inayofuata na tuweze kuwa na indicator mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu katika hali ya kawaida, tutazungumza kwamba hali ya uchumi inakuwa lakini utaona bado tunaweza kuwa na maswali mengi ambayo tunaweza kujiuliza. Kwa sababu kutakuwa kuna gape kati ya nominal income na real income hasa kwenye maisha yale ya kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba wakati tukizungumza juu ya kukua kwa hali ya uchumi lakini ukienda kule chini utaona kabisa kwamba bado kuna hali isiyo nzuri. Kwa hiyo Idara hii ya Takwimu iwezeshwe ili basi takwimu zinavyokuja hapa tuweze kuona zinaenda na hali halisi. Utaona kabisa kwamba kama ni mishahara itaonekana haitoshi kulingana na hali ya maisha, utaona kama ni bei ya mazao haitoshi kulingana na maisha. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiria kwamba Idara ya Takwimu iwezeshwe ili iweze kuleta uhalisia.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakuja kuona kwamba bado tuna income gape kwenye society, kwa hiyo, tuone hili gape likizibwa ili lisitupe nafasi ya kuburuza wale wanaoishi maisha ya hali ya uduni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuangalia kwenye kitabu cha hali ya uchumi, kumbukumbu nyingi zinaonesha zimechukuliwa hasa katika maeneo ya mjini, na sehemu kubwa utaona majedwali yanaonesha hali hii imechukuliwa katika masoko ya Dar es Salaam na yameacha kuchukua maeneo ambayo pia yametajwa kwamba ni maeneo ambayo yana umasikikini mkubwa, wananchi wanaishi chini ya mstari ule wa umaskini. Kwa Mikoa kama Kigoma, Geita, Kagera, Singida, Mwanza utaona kwamba upo umuhimu sasa hizi data zichukuliwe kwenye maeneo haya zikichanganywa na maeneo mengine, ili tukipata wastani uwe wastani ambao utakuwa unagusa wananchi walio wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nizungumze juu ya hii dhana ya ukuaji wa uchumi kwa ujumla hii; kwamba tunataka twende kwenye uchumi wa viwanda, tuwe na uchumi wa kati. Sasa nilikuwa najaribu kujiuliza, kwa sababu kama Mheshimiwa Waziri wakati anamalizia kusoma hotuba yake alizungumza juu ya umuhimu wa wananchi wote kutakiwa kushiriki katika kuhakikisha kwamba uchumi unakua. Lakini walio wengi tunaweza tusielewe tunavyozungumza juu ya tunahitaji kwenda kwenye uchumi wa kati. Je, wastani wa pato kwa mtu unatakiwa uwe wapi, iwe ni dola 1,500 kwa mtu au 3,000 kwa mtu?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo yako mambo ambayo tunahitaji pia ili wananchi wetu kwa ujumla, ambao pia kila mmoja ana mchango wake katika ukuaji wa uchumi, aweze kuelewa kwamba tunataka twende kwenye uchumi unaotegemea viwanda na biashara. Tunahitaji pia wastani wetu wa kipato kupanda kwenda dola 3,000 kwa mtu kufika mwaka 2025; kila mwananchi aweze kushiriki katika ujenzi wa uchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, na hii pia itawezesha wananchi wetu wengi ambao bado hawajapata ajira, wapate ajira ili waweze kushiriki vizuri katika ujenzi wa uchumi. Lakini pia bidhaa zetu tutakazozizalisha katika viwanda ziwe na ubora kiasi cha kumudu ushindani katika masoko ya dunia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni muhimu sana jambo hili litafsiriwe vizuri, wakati mwingine Wizara ifanye utaratibu wa kutoa vipeperushi virahisi ili wananchi mpaka aliyeko huko chini aweze kujua kwamba kwa pamoja tunaelekea wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, nilipenda nishauri kwamba ni vyema tutafsiri vizuri ili wananchi waelewe, na hasa watumishi walioko kwenye Halmashauri na watumishi wengine, waweze kuijua hii dhana nzima ya kwenda kwenye uchumi wa kati na wa viwanda, na hivyo tuweze kuielewa vyema na kushiriki ujenzi wa uchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme kwamba Serikali imechukua hatua nzuri kwa sababu hapo nyuma tulikuwa na matatizo makubwa ya kutokukusanya kodi kiasi cha kutosha. Sasa inaonesha kabisa kwamba Serikali inafanya juhudi kubwa ya kufanya makusanyo. Ukiingalia hii bajeti ambayo imekuja leo utaona kabisa kwamba ipo dhamira ya Serikali ya kufanya tutegemee mapato yetu ya ndani; hili ni jambo la kupongeza sana Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kulikuwa na tatizo la kutokutolewa kwa mafungu, kwamba mtiririko wake haukuwa mzuri. Naamini kama juhudi za makusanyo zitaongoezeka kile ambacho tumekipitisha hapa kikiweza kufika na kwa wakati tutayaona maendeleo kwa haraka. Pia ninaona Serikali ina dhamira ya dhati kwa kusimamia nidhamu ya makusanyo na matumizi. Mwanzo ilikuwa ni shida lakini kwa hali iliyoko sasa hivi inatutia matumaini kwamba tunakwenda kwenye mwelekeo mzuri. Kwa hiyo, nishauri tu, tuweke hamasa kubwa kwenye makusanyo ya mapato ya ndani ili tuweze kujitegemea, lakini pia tusimamie nidhamu katika ukusanyaji na matumizi ya rasilimali zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nizungumze kidogo juu ya sura ya bajeti. Kuna mambo ambayo nilikuwa nafikiri niweze kushauri. Kwanza napongeza ukuaji wa bajeti hii, kutoka trilioni 22 kwenda trilioni 29, si jambo dogo, ongezeko la zaidi ya asilimia 23, ni jambo la kuipongeza Serikali. Pia uwiano wa matumizi ya kawaida na matumizi ya maendeleo umeongezeka. Nilikuwa nafikiria kwamba tuiangalie vizuri kwa baadhi ya maeneo, kwa mfano kwenye Halmashauri zetu au Serikali za Mitaa bajeti ya maendeleo iongezwe. Kwa sasa hivi tuna kama trilioni 1.3 ambayo tunaipeleka kwenye Serikali zetu za Mitaa. Hali itakapokuwa nzuri tusukume hizi pesa za maendeleo ziende zaidi kwenye Serikali zetu za Mitaa ili isaidie kuondoa baadhi ya matatizo yaliyo mengi huko.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahishwa pia na juhudi za Serikali kuangalia suala zima la usimamizi wa kodi. Kwa hiyo, ni…
NAIBU SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa Kwandikwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi na ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ameniwezesha kusimama kwenye Bunge lako hili. Pia nishukuru kwa dhati Wizara hii ni Wizara ambayo mimi nimefanya kazi nikitumika katika Ofisi ya Taifa ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kwa hiyo, kufika kwangu hapa kwa moyo wa dhati naamini uko mchango mkubwa wa Wizara hii.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwamba Wizara hii inasimamia mafungu mengi na kama tulivyoona kwenye report hii kuna mambo mengi ambayo ameyaonyesha Mheshimiwa Waziri niwashukuru kwa kazi nzuri ambayo inaendelea kufanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niende moja kwa moja kwenye kuchangia hoja hii. La kwanza nilitaka nijue tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Rais hapa aliahidi kwamba Sheria ya Manunuzi italetwa katika Bunge hili. Nilikuwa nikipitia report, sijaona kwamba tumejiandaa namna gani ili sheria hii ambayo ni mwiba inakuja kwenye Bunge hili ili tuweze kuipitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilitaka nizungumze juu ya hizi idara chache tu ambazo ziko chini ya Wizara hii nikianza na hii ya Ofisi ya Msajili wa Hazina. Utaona kabisa kwamba inalo jukumu kubwa sana la kusimamia taasisi nyingi ambazo ziko chini yake na hizi taasisi tunategemea zikisimamiwa vizuri ili ziweze kutoa mchango mkubwa wa mapato katika Serikali. Niko kwenye Kamati ya Uwekezaji ya Mitaji ya Umma, utaona kabisa kwamba mashirika yaliyoko huko na taasisi ziko 215 lakini tunahitaji tuwe na watumishi wengi sasa utaona kabisa hata bajeti ta TR iko ndogo sana na bado tumeona hapa, tumesikia kutoka kwenye taarifa ya Kamati wamepata asilimia nane ya kilichokuwa kimebajetiwa kipindi kilichopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji kuangalia mambo mengi sana katika taasisi hizi ili ziweze kutoa mchango mkubwa kwenye mfuko mkuu wa Serikali. Capital structure ya mashirika haya haiko vizuri, lakini utaona mashirika yaliyo mengi hata investment plan hayana, kwa hiyo, utaona tunahitaji watu wenye weledi tofauti katika ofisi ya TR ili iweze kuweka msukumo mzuri na mwisho wa safari tuone mchango mkubwa unakwenda kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ukiangalia kwenye kiasi ambacho kitachangiwa na non-tax revenue bado kiasi hiki ni kidogo lakini ukienda kuangalia kwa undani kabisa nafasi ipo kama tutasimamia vizuri Mashirika haya naamini kwamba mchango mkubwa utakuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilitaka nichangie tu kwenye hii Wizara, kwamba nilikuwa nafikiria Mheshimiwa Waziri atasema hii kada ya wahasibu. Kada ya wahasibu bado inatoa tu taarifa, msukumo haujawekwa vizuri nilikuwa nafikiria labda tungeweza kuzipandisha hadhi angalau ziwe katika hadhi ya Ukurugenzi ili waweze kutoa mchango mkubwa wa uchambuzi lakini pia kushiriki katika maamuzi kwenye Wizara. Kwa hiyo, utaona tumeendelea kuwa na unit, lakini umeona kabisa katika Wizara kuna fedha nyingi sana ambazo Wahasibu wanasimamia nilikuwa nafikiri Mheshimiwa Waziri alitazame. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine nilitaka nizungumze juu ya uandaaji wa hesabu. Serikali imefanya uamuzi mzuri utayarishaji wa hesabu kwa viwango hivi vya Kimataifa kwenye Accrual Basis, utaona sasa karibu kile kipindi cha mpito karibu kinakwisha, hatutakuja kuwa na hesabu nzuri. Tunahitaji tupate hesabu ambazo zitaonyesha ile National Wealth tuone majengo yanaonekana kwenye hesabu, jumuifu tuone madaraja gharama zake, tuone ardhi, tuone madeni na mali mbalimbali, utaona sasa tangu tulivyoingia kwenye mfumo huu ikifika mwaka 2017 itakuwa kile kipindi cha mpito kinaisha, tutategemea kuwa na hesabu ambazo zinaweza zisipate hati safi kama ilivyokuwa kwenye Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa liko jambo la kufanya Mheshimiwa Waziri, uliangalie hili, kikubwa zaidi kwenye kufanya uthamini wa mali utaona kwamba hata Kwenye Halmashauri za kwetu tunao ma-valuer lakini hawafanyi kazi ya kutathmini mali hizi za Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nafikiri nimshauri Mheshimiwa Waziri kwamba hili suala la kuthamini mali lichukuliwe kama ni National issue ili tuwe na frame work nzuri ya kuhakikisha kwamba tuna muda wa haraka kukamilisha uthamini wa mali ili hesabu zetu siku za usoni ziweze kuwa nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niliombe kupitia Wizara yako Mheshimiwa Waziri, mafunzo ya IPSAS kwa sababu update zipo kila wakati, tuweke msukumo ili tuweze kuwa na hesabu nzuri ambazo zitatusaidia kufanya maamuzi mbalimbali tunahitaji kuwa na kuhasibu oil and gas, tunahitaji kuhasibu shares na investment, kwa hiyo kila wakati kuna update zinakuja nilikuwa najaribu kuangalia kwenye bajeti ninaona kwamba saa nyingine upande wa mafunzo bado kidogo tunahitaji tuweze kusukuma tuweze kuweka mafungu ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilitaka nizungumze juu ya accountability (uwajibikaji). Nilikuwa najaribu kuzitazama hizi ofisi za Internal Auditor General lakini naangalia pia na ofisi ya CAG. Nilivyokuwa nikiangalia kule naona kwamba tutakuwa na shida kubwa kwa sababu pamoja na kuwa kulikuwa na utaratibu ule wa kupunguza matumizi kwenye OC lakini utakuja kuona kabisa kuna kazi hazitafanyika. Mheshimiwa Waziri alitazame hili, Internal Auditor General ofisi yake ikiwezeshwa, itamuwezesha CAG iwe nyepesi na saa nyingine hata gharama za ukaguzi zinaweza zikapungua lakini bado naona hapa msukumo upo mdogo, hivi kwa nini Mheshimiwa Waziri ofisi ya Internal Auditor General isipewe full vote ili uwajibikaji uweze kuongezeka? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia bajeti ya CAG imepungua sana na ukija kuiangalia kwa undani nilikuwa naangalia kitabu Volume II, utaona kabisa kwamba hizi kaguzi kwenye Serikali za Mitaa hazitafanyika Mheshimiwa Waziri hebu litazame kwa sababu utaona kwamba imetengewa kwenye ule upande tu wa kwenda kutembelea Halmashauri, kwa mfano, ziko shilingi milioni 332 kwenye kile kifungu ukiangalia. Sasa hii ni wastani tu labda wa mtu mmoja siku 20 kila Halmashauri ataenda kufanya kazi haitawezekana, kwa hiyo utaona kabisa kwamba hii funding iliyokuwepo kwenye ofisi hii Mheshimiwa Waziri itazame vizuri lakini vinginevyo hatutategemea kuwa na report nyingi kama ulivyozionyesha kwenye report hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna report nyingi sana mwaka huu tumezipokea, kwa hiyo tutegemee siku za usoni hatutakuwa na report za ukaguzi nyingi kama ilivyokuwa kwa sababu hali iliyopo hapa siyo nzuri. Utaona kabisa sehemu ambayo ilikuwa imetengewa kwa mwaka uliotangulia shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya ukaguzi wa Wizara, ziko shilingi milioni 280, sasa hii inatuonyesha nini? Inaonyesha kwamba hii kazi ya ukaguzi haijapewa msukumo wa kutosha ili kuhakikisha kwamba tunapata report lakini mwisho wa safari tunaweza kufanya maamuzi mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka pia nimalizie kwa kutoa ushauri tu kwamba kama tulivyosikia kwenye report ya Kamati pia kwamba kiasi ambacho kilikuwa kimetengewa kwenye bajeti ni kiasi kidogo, kwa hiyo, wakati msukumo mkubwa unakwenda kufanya makusanyo ya kutosha basi tuhakikishe kwamba kiasi ambacho kinatengwa kwenye Bunge lako hili Tukufu kinapelekwa na kwa wakati ili kama kiasi chote kitatolewa basi itakuwa ni wakati mzuri wa miradi mbalimbali ya maendeleo kuweza kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati huo huo tuendelee kuangalia maeneo mengine ambayo yataweza kuongeza mapato ya Serikali na hasa hasa hii non-tax revenue yako maeneo mengi ambayo tukiweza kuweka msukumo mkubwa tutaweza kuona kwamba tunapata fedha za kutosha na mwisho wa safari utaona kwamba angalau hata ule mtiririko wa fedha kwenda kwenye Halmashauri utakuwa unakwenda vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusisitiza tena suala la asset valuation ni suala muhimu sana ili national accounts ziweze kuficha vizuri ili mali zetu kwenye Halmashauri zetu ziweze kuonekana vizuri, lakini pia hati safi ziweze kuongezeka. Utakuja kuona kwamba kwenye Halmashauri zetu kwa mwaka huu uliokwisha saa nyingine tunaweza tusiwe tumefanya vizuri sana lakini kutokana na hili tatizo kubwa la asset evaluation imekuwa ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimia Naibu Spika nashukuru sana kwa nafasi hii naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye taarifa za Kamati ya PAC na LAAC. Nianze kwanza kuishukuru Serikali kwa hatua mbalimbali ambayo imekuwa ikizichukua ili kuweza kupunguza yale mapungufu mengi ambayo yalikuwepo kipindi cha nyuma. Tumeshuhudia kumekuwa na reforms mbalimbali hususani financial management reforms zenye lengo la kuleta udhibiti wa matumizi ya Serikali, lakini pia kuondoa mapungufu mengi ambayo yamekuwa yakijitokeza siku za nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine kumpongeza CAG na wafanyakazi walioko chini yaOfisi ya CAG kwa sababu taarifa hizi ambazo tumeletewa ni matokeo ya kazi nzuri ya CAG ambayo ameifanya. Wachangiaji wengi wamekuwa wakizungumza juu ya mapungufu yaliyokuwepo, kikubwa yanasababishwa na ule udhibiti wa ndani, lakini kama nilivyosema kwamba Serikali imeanzisha pia Ofisi ya Internal Auditor General kwa nia hiyo ya kuleta udhibiti madhubuti kwenye taasisi zetu na mashirika yetu na hasa hata kwenye Serikali zetu za Mitaa. Kwa hiyo, naona Serikali imekuwa ikifanya juhudi kubwa na naamini kwamba kadri tutakavyokwenda mambo yataendelea kuwa mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa ya ukaguzi ni kututhibitishia kwamba rasilimali za umma, zile asset za umma ziko katika hali nzuri, lakini pia tunapata ushauri kutokana na ukaguzi na matokeo yake ndiyo kama hivi kwamba Kamati zetu zimepata input ya kuweza sasa kuliletea mapendekezo Bunge ninaunga mkono mapendekezo yote ambayo yapo kwenye Kamati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite zaidi kwenye mashirika ya umma. Niko kwenye Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma. Nilitaka nizungumze machache kuhusu ufanisi ambao utatekeleza saa nyingine haya mashirika ya umma kuweza kupunguza matatizo yaliyokuwepo lakini pia kuweza kuongeza mapato, non-tax revenue katika Serikali. Kwa sababu ukiangalia bado ule mchango ambao unakwenda kwenye Serikali kwenye mapato bado uko mdogo, ukiangalia kwenye bajeti ya 2016/2017, mchango huu ambao ni non-tax revenue ukijumlisha pamoja na Halmashuri uko asilimia 11.3; lakini ukiona kwenye mwaka huu ambao tunakwenda kuzungumzia kipindi kijacho projection iko asilimia 12.35. Kwa hiyo, bado mchango uko mdogo kwa hiyo, ninaamini kwamba kuna mambo mengi yakishughulikiwa hasa hasa kuboresha mashirika yetu, mchango utakuwa mkubwa katika Pato lile la Taifa.
Mhesimiwa Naibu Spika, nizungumze mambo mawili, jambo la kwanza nilitaka niseme kuhusu kuwezesha Ofisi ya Msajili wa Hazina. Utakuja kuona kwamba Msajili wa Hazina amekuwa akifanyakazi kubwa kwa upande wa Mashirika ya Umma lakini pia kwenye upande wa PAC naamini kwamba amekuwa kitoa mchango wao kuwezeha kazi za Kamati kufanyika vizuri. Lakini bado liko jambo la kumwezesha huyu Msajili ili aweze kupata uwezo mkubwa wa kufanyakazi na kuweza kusimamia mashirika haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaona kwamba kazi ya kwake ya kushauri mashirika juu ya uanzishwaji na hata saa nyingine kufutwa baadhi ya mashirika ambayo hayana ufanisi lakini liko jambo pia la kuangalia ule utendaji wenye tija katika mashirika. Kupitia mipango na bajeti za mashirika na hata jana umeshudia tumepitisha mabadiliko ya sheria kwa nia ya maana kusaidia katika mashirika haya ili kuwa na uwiano ule wa matumizi na mapato yanayotoka kwenye mashirika haya hii itaiwezesha Serikali kuweza kupata gawiwo au fedha kutoka kwenye mashirika yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini anayo majukumu mengi, hii ni pamoja na kuweka viwango vya mashirika yetu kuweza kufanya makusanyo, lakini pia kuweza kuzisimamia hizi Bodi za Mashirika, kusimamia management na Kamati zake. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiria nipendekeze tu kwamba Serikali iitazame hii ofisi ya Msajili wa Hazina ili iweze kusaidia kuleta tija na kupunguza mambo ambayo yamejitokeza katika mashirika yetu ambayo yana changamoto nyingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika mashirika yetu ukiingalia sura ya mitaji iliyoko kwenye mashirika yaliyo mengi sura yake siyo nzuri inahitajika ifanyike uchambuzi wa makusudi wa nguvu na kushauri ili tuweze kuona zile capital structure kwenye mashirika yetu zinakuwa ni nzuri lakini kunahitaji pia kuweza kuona kwamba kuna mambo ambayo yameonekana kwenye report hii kwamba kuna madeni mengi kwa mashirika ambayo yanakusanya mapato yameshindwa kukusanya mapato vizuri, ipia utakuja kuona kwenye mizania kuna matatizo kwamba kuna rasilimali au asset za mashirika haya hazijafanyiwa evaluation muda mrefu, utaona matatizo yako mengi, iko ile mikakati ya kuweza kudhibiti vihatarishi (risk management) katika haya mashirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nafikiria niliseme hili kwamba Serikali iangalie sana hii ofisi. Ofisi inayo majukumu mengi na kama itawezeshwa kwa maana ya kuweza kuhakikisha kwamba wamekuwa na rasilimali za kutosha ili kuweza kushughulikia mashirika haya, tutaona kwamba tutaweza kuongeza ufanisi katika haya mashirika ambayo yapo kwa sababu ukija kuangalia mashirika yaliyo mengi hawana investment plan, mashirika yaliyo mengi utaona hakuna risk strategy za kuweza kuondosha hatari ambazo zinafanya mashirika haya yasiwe na ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, haya yote haya Msajili wa Hazina anatakiwa kuyatazama na kwa kasi kubwa ili tuweze kuondokana na hayo matatizo ambayo yapo. Utakuja kuona hata kuna taasisi zingine za kifedha ziko chini ya Msajili wa Hazina na zenyewe zimekumbwa na matatizo haya ya kutokupata faida. Kuna mikopo chechefu, lakini pia ule uwekezaji lazima usimamiwe vizuri ili tuone kwamba mashirika haya yanaweza kufanya vizuri. Kumekuwana pia kutokuwa na record nzuri kwenye hesabu, kuna over statement za asset au under statement kwa hiyo haya mambo hayo ni muhimu sana yaweze kutazamwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la internal control, udhibiti wa ndani ni muhimu sana kutazama katika maeneo yote ili tuweze kupunguza hizi hoja lakini kikubwa tuweze kuwa na ufanisi mzuri katika kusimamia hizi rasilimali. Kwa hiyo, nilitaka nishauri tu kwamba jambo la kwanza Serikali isisitize sana kuhakikisha kwamba kunakuwa na Kamati za Ukaguzi ambazo zinatakiwa ziimarishwe, ziwe na watu wenye weledi lakini kama itawezekana pia kwenye mabadiliko ya sheria zetu tuzitazame ili Wajumbe wa Kamati hizi za Ukaguzi waweze kutoka nje ya taasisi husika ili ule ushauri uweze kusaidia kuboresha mashirika yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la lingine; wakaguzi wa ndani utakuja kuangalia hata katika Halmashauri zetu wakaguzi wa ndani ni wachache. Unakuta wakati mwingine wakipata fursa ya kwenda kwenye mafunzo ofisi zinafungwa zina wakaguzi wawili, zina wakaguzi watatu na hawa wakaguzi wa ndani ni jicho kwenye management iweze kusaidia kurekebisha mambo mapema kabla mambo hayajaharibika.
Kwa hiyo, ni muhimu Serikali itazame, imuwezeshe Mkaguzi mkuu wa ndani lakini pia wakaguzi wa ndani walioko kwenye taasisi zetu waweze kupata mafunzo lakini pia waweze kuongezwa ili waweze kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kuangalia pia kuwezesha mashirika yetu yana upungufu wa fedha, Serikali kama inaweza kwa sababu imekuwa ikiongeza makusanyo tuanzishe huu mfuko wa uwekezaji ili uweze kusaidia mashirika na taasisi ambazo ziko chini ya TR ili ziweze kuweza kupata fedha kutoka kwenye mfuko huu. Tuyaimarishe haya mashirika ili mwisho wa siku yaweze kuongeza gawiwo upande wa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kukushukuru kwa kunipa nafasi hii kilio changu kikubwa ilikuwa ni kuhakikisha kwamba Ofisi ya TR inawezeshwa ili ikiungana na taasisi nyingine zinazoshughulikia masuala ya uadilifu, masuala haya ya tija, ziweze kufanya vizuri ili mwisho wa siku hoja zipungue lakini kikubwa ziweze kuchangia kwenye maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuunga mkono hoja. Naomba Serikali itengeneze mnyororo wa huduma na kuhudumiana (chain supply) ili uzalishaji wa viwanda vyetu ulenge kwanza kuhudumia mahitaji ya ndani (soko la ndani). Yapo mahusiano kati ya viwanda, masoko na ubora wa miundombinu ya umeme, maji, barabara, mawasiliano na uzalishaji wenye tija. Hivyo namwomba Mheshimiwa Waziri awasiliane kwa karibu na Wizara nyingine ili kuwe na matokeo chanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri elimu itolewe ili wananchi na wataalamu, viongozi waliopo vijijini waelewe viwanda vinaanza na viwanda vyenye kuajiri watu 1, 2, 3, 4 - 9 hadi viwanda vikubwa. Wananchi hawaelewi kama shughuli wanazofanya kama usindikaji wa vyakula ni viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utunzaji wa data, naishauri Wizara iwe na utaratibu wa kuweka kumbukumbu (data) ili kuweza kuchambua maendeleo ya uendeshaji viwanda na matokeo yake kama vile idadi ya walioajiriwa Kiwilaya hadi Kivijiji. Hii itasaidia kufanya maboresho ya mara kwa mara. We need to have proper and useful information.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nashauri utafiti ufanyike mara kwa mara ili Wizara iweze kutoa ushauri, maagizo na maelezo ya namna Sera ya Uchumi wa Viwanda uweze kutekelezeka. Utafiti ufanyike pia ili tujue changamoto za uendeshaji wa viwanda na utatuzi wa changamoto kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la ufafanuzi kwa Waziri: Je, Mheshimiwa Waziri, Wizara ina mpango gani wa kuhimiza ushirika na wenye viwanda hususan viwanda vidogo vidogo ili iwe rahisi kuwafundisha kupima maendeleo yao na kuona kwa kiasi gani viwanda vimepunguza hali ya umasikini na kuongeza ajira?
Je, Mheshimiwa Waziri ana mpango gani kuhimiza mafunzo ya uendeshaji viwanda kwa ufanisi hususan Jimboni Ushetu?
Je, tutawatumiaje vijana waliohitimu mafunzo ambao hawana ajira kushiriki na kutumika katika ukuzaji wa viwanda?
Je, Sekta ya Viwanda inapunguza kwa kiasi gani mfumuko wa bei kwa kusogeza huduma ya masoko karibu na wananchi?
Je, hadi sasa kuna changamoto zipi za kiteknolojia kifedha, kisera na kiutawala ambazo bado hazijatatuliwa na zinazokwamisha maendeleo ya haraka katika viwanda vyetu na kwa namna gani changamoto hizi zitatatuliwa?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia makadirio ya Ofisi ya TAMISEMI na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, nitumie nafasi hii nimshukuru sana Mungu ameniwezesha kuingia kwenye nyumba hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nikupongeze sana wewe mwenyewe kuchaguliwa kuwa kiongozi wetu. Niseme najivunia kuwa Mbunge wa Jimbo la Ushetu na najivunia pia kuwa na Madiwani wote wa Chama cha Mapinduzi. Nilikuwa napata shida kidogo na maswali, watu wengine hawajui Jimbo la Ushetu liko wapi, Jimbo la Ushetu limetokana na lile Jimbo la Kahama. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya. Mheshimiwa Rais ametupa Baraza zuri la Mawaziri, Mawaziri ambao wanatusikiliza na naamini kwamba watafanya kazi vizuri kwa maendeleo ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Chama cha Mapinduzi kimetupa ilani nzuri sana. Niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge ambao labda hawajaipitia vizuri waisome, ni msingi mzuri wa kwenda kwenye maendeleo na kasi ambayo tunaihitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sikupata nafasi ya kuchangia kwenye Mpango wa Pili wa Maendeleo lakini nitumie nafasi hii niseme kwa ufupi kabisa kwamba nilisoma Mpango wa Maendeleo umezingatia sana Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini pia umeangalia sana kwenye ule MKUKUTA. Kwa hiyo, niipongeze sana Serikali kwa kutazama kwa umakini na uhakika Mpango huu kwa madhumuni ya kuwaletea maendeleo wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kwa ujumla juu ya Halmashauri zetu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri Simbachawene kwa kazi ambayo anaifanya. Nina uhakika kwenye mpango huu aliouleta utakapokwenda kufanyika kuna mambo mengi ambayo tutakwenda kufaidika nayo sisi wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kwanza suala la kuzisaidia Halmashauri zetu kuhusu watumishi. Rasilimali watu ni muhimu sana kwa sababu ndio rasilimali ambayo itakwenda kusimamia rasilimali zingine, itakwenda kusimamia rasilimali fedha na mambo mengine ya kiutekelezaji. Kwa sababu ukija kuangalia, TAMISEMI ndiyo Wizara ambayo inakwenda kusimamia mambo mengi ambayo pia yatakuwa yameonekana kwenye Wizara zingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nishauri tu kwamba, Serikali itazame eneo hili la watumishi pamoja na namna ambavyo inachukua hatua mbalimbali za kuweza kuhakikisha kwamba watumishi wa umma wanakuwa na nidhamu lakini lazima tupeleke msukumo mkubwa kuhakikisha kwamba tunawapa weledi wa kutosha watumishi wetu, tunakuwa na idadi ya kutosha lakini pia tuangalie kama tunaweza kuwapa motisha ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi ili kuendana na kasi hii ya Rais wetu ya kuchapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nizungumzie juu ya mapato, uko umuhimu wa kutazama sana katika hizi Halmashauri zetu. Nilikuwa nikiangalia kwenye majedwali ya namna ambavyo fedha zimekuwa zikienda kwenye Halmashauri zetu lakini pia nimeangalia na ongezeko la makusanyo, ningependa nimshauri Mheshimiwa Waziri tuweze kuongeza ruzuku kwenye Halmashauri zetu. Kwa sababu ukisoma kwenye mtiririko wa fedha inaonekana kwamba ruzuku zimekuwa zikishuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa hesabu kuanzia za mwaka 2013/2014, Halmashauri zimekuwa zimetengewa shilingi bilioni 704, mwaka uliofuata 2014/2015 zilitengewa shilingi bilioni 563 na mwaka wa fedha uliofuata Mkuu ya mwaka wa fedha 2011/2012, kati ya wilaya ambazo zilikuwa zimekuwa proposed kuanzishwa ni Wilaya ya Ushetu lakini haikuanzishwa kwa sababu hatukuwa na halmashauri. Sasa tunayo halmashauri ambayo ilianzishwa mwaka 2012 na sasa tunalo jimbo na ili tuendane na maendeleo ambayo tunahitaji, tunahitaji kwa kweli tupate wilaya. Yako mambo mengi ambayo yanatupita kutokana na ile dhana tunapokuwa tunayapeleka maendeleo tunayapeleka kwenye Makao Makuu ya Wilaya tunasahau kwenda kwenye halmashauri ambazo haziko kwenye Makao Makuu ya Wilaya ambako ndipo watu wengi walipo. kwa hiyo, nafikiri hili linaweza kuwa ni changamoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mtizamo uwe kuangalia huduma zinaenda kwa wananchi walio wengi ambao wako nje ya makao Makuu ya Wilaya. Kwa hiyo, napenda niombe sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili kwa sababu ni muda mrefu tumechelewa kupewa Wilaya kwa sababu ya kutokuwa na Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengine ya huduma ambayo kwa sehemu kubwa kama nilivyozungumza Serikali zetu za Mitaa ndiyo zinasimamia pamoja na kuwa yanasimamiwa na Wizara zinahusika lakini ile manpower kubwa iko katika halmashauri zetu. Nikianza na eneo la afya tupate fedha za kujenga Hospitali ya Wilaya ya Ushetu.
Mheshimiwa Naibu, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Ushetu halikubahatika kujengewa miundombinu ya umeme. Tumepata vijiji viwili tu. Tunao uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na misitu na tunahitaji kuchakata mazao yetu ili tuinue uchumi wa wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumehamia Makao Mapya ya Halmashari ya Ushetu ambayo yako katika Kata ya Nyamilangano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yangu Mheshimiwa Waziri, tupelekewe umeme kwa haraka Makao Makuu ya Halmashauri yetu ya Ushetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tujengewe miundombinu ya umeme kwenye vijiji vyote REA II ili tuweze kuchangia katika kukuza viwanda na uchumi wa nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, Mheshimiwa Waziri nakushukuru kwa ushirikiano wako na nia yako thabiti kutusaidia wana Ushetu. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la malisho katika Jimbo la Ushetu, napenda kushauri na kuomba Wizara iturejeshee msitu wa Usumbwa uliochukuliwa na Serikali mwaka 2002 ili wananchi wapate sehemu ya malisho na kushiriki kikamilifu kuhifadhi Mbuga ya Kigosi-Moyowosi. Ushetu tumeanza kutoa hamasa ya wananchi kushiriki katika hifadhi kwa kutozana faini za kimila ili kuzuia uharibifu, shida yetu ni eneo la malisho.
Pili niombe na kushauri tupewe eneo la msitu wa akiba wa Ushetu/Ubagwe ili tupate eneo la malisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirikiano; naomba sana Wizara itoe ushirikiano kwa wananchi na Wabunge wanaopakana na hifadhi, mashirika mbalimbali ikiwemo ya dini, vikundi na uongozi wa kimila ili tuzungumze namna bora ya kutatua migogoro katika maeneo yetu baina ya wahifadhi na wananchi ama wafugaji.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia huu Mpango wa Maendeleo. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa sababu ukiuangalia kwa ujumla mpango huu, nimeusoma vizuri na pia niseme kwamba nimechangia kwa maandishi kwa sababu ya muda. Mpango huu ni mzuri kwa sababu mpango huu ni muendelezo wa ule mpango wa miaka mitano. Kwa hiyo ukiusoma vizuri utaona kabisa kwamba uko mwendelezo mzuri, sasa kuna mambo kadhaa ya kufanya, ambayo nilikuwa napenda kushauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu umezingatia Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini pia umezingatia mpango wa maendeleo endelevu. Kwa hiyo, nilikuwa nataka ni- appreciate kwa kuona kwamba kwa kweli ukiangalia hali ya uchumi kwa ujumla kwa taarifa ilitolewa na BOT mwezi Agasti, utaona kabisa kwa performance ya bajeti ya Julai, maendeleo ni mazuri, kwa hiyo, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende tu moja kwa moja kwenye ushauri, nilikuwa napenda nishauri mambo kadhaa, ambayo tumeyaona kama changamono na Waheshimiwa wengi wamechangia hapa. Ipo changamoto ya ukusanyaji kodi kwamba yako maeneo kama mpango unavyosema kwamba unakwenda kutazama sekta binafsi, lakini pia tumezungumza juu ya kuendeleza viwanda, lakini uko uhusiano mkubwa kati ya sekta binafsi na ukuaji wa viwanda na suala la ukuaji wa uchumi kwa ujumla. Kwa hiyo kuna mambo ya kuyaangalia hapa ili sasa tuweze kusaidia sekta, Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia maeneo haya ya kodi, kwa sababu ukweli lazima wafanyabiasha na sekta binafsi walipe kodi. Lakini kuna maeneo ambayo ni ya kuyatazama ili kuweza kufanya ile tax compliance iwe ya hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia kwa mfano, upenda wa VAT kwenye viwanda vyetu ambavyo vipo kwa mfano, viwanda ambavyo vinasindika mafuta, mashudu yale yamewekea VAT, utakuja kuona kwamba VAT register ni kama agent wa TRA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapokuwa na hii VAT kwenye uzalishaji wa kwanza utaona inavutia kuongeza bei na kwamba ule ushindani sasa wa bei unakuwa ni mgumu kwa product inayofanana na wenzetu nje ya nchi na hata kwa watumiaji wa bidhaa hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tulitazame hili suala la namna ambayo kodi itahamasisha ili ule ulipaji wa kodi, compliance iwe kubwa kwamba mtu alipe bila kushurutishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lipo nilitaka nishauri, kumekuwa na tatizo hili la mzunguko wa fedha. Sasa nilikuwa najaribu kufikiria kwamba tulikuja na sheria ya bajeti ili mwezi ule wa saba kuwe na kiasi cha kutosha cha fedha kuweza kuendesha bajeti zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kunahitajika kutazama hili suala la cash flow management, Wizara ilitazame ili tunapokuja kupitisha bajeti mwanzoni mwa mwezi wa saba kuwe na flow nzuri ya fedha kulingana na uhitaji katika maeneo mbalimbali, katika Halmashauri zetu. Kwa hiyo, sikuona tatizo sana kwa sababu kama bajeti ipo na fedha inayotolewa iko within the budget, hapa hakuna shida, ila lipo suala la kuangalia ile flow ya pesa inayokwenda kwa ajili ya matumizi, kwa hiyo, Wizara hapa iangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mzunguko wa fedha, hili linaonyesha kwenye sekta ya fedha, Wizara ilitazame kwa sababu kunapokuwa na mabadiliko ya hizi sheria za kodi zilivyokuja, lakini pia mabadiliko katika taasisi zetu za kifedha, watu wanapata hofu ya kupeleka fedha katika hizi taasisi za fedha. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba zile deposit kwenda kwenye mabenki zimepungua kiasi kwamba ule mzunguko umepungua. Kwa hiyo, sasa BOT iangalie namna yaku-regulate ule mzunguko wa fedha ili tuione inaleta impact kwenye mzunguko na ukuaji wa uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uko uhusiano mzuri sana kati ya sekta binafsi na ukuaji wa viwanda, sasa uko umuhimu pia wa kuliangalia suala la kilimo. Kilimo chetu hakijapewa msukumo wa nguvu ili kuhakikisha kwamba sasa tunapata raw material za kutosha kuendesha viwanda vyetu. Ukija kuangalia kwenye zao la pamba, uzalishaji wa pamba umeshuka, katika msimu huu ununuzi wa pamba umefanyika kwa wiki mbili tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuta sekta binafsi watu wana viwanda vyao vya kuchambua pamba vimesimama mtu ambaye alitakiwa kununua tani 60,000 katika msimu huu amenunua tani 14,000 utaona kabisa kwamba tuna dead asset, ziko asset za wafanyabiashara hazisaidii mchango katika uzalishaji. Kwa hiyo, Wizara itazame namna gani ya kuweza kusaidia haya maeneo ili tuwe na uwiano mzuri kati ya uzalishaji katika kilimo, uzalishaji katika viwanda vyetu ili tuweze kuhakikisha kwamba nchi yetu inapata fedha za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Serikali ijaribu kuangalia kusaidia tuje tupate kiwanda ambacho kita-support hivi viwanda vidogo ambavyo vipo vinachambua pamba, tupate kiwanda kikubwa kwa ajli ya kutengeneza nguo ili pia sasa tuweze kuzalisha nguo za kutosha ili wananchi wa Tanzania waweze kupata nguo kwa bei ambayo inakuwa ni nafuu na kufanya kwamba hali ya uchumi iweze kuwa nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka pia nimalizie kutoa ushauri kwamba tulipokuwa tumeanzisha mfumo wa usimamizi wa fedha tumekuja na hii concept ya accrual basis, sasa…
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono, ninashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hoja hii ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nianze kwa kuunga mkono hoja. Pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa namna ambavyo ameanza kwa kuonesha juhudi ya kuweza kuhakikisha kwamba rasilimali hii muhimu inakuwa katika hali ambayo inalineemesha Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana wananchi wa Jimbo langu la Ushetu kwa sababu tumekuwa na matatizo makubwa sana, lakini wamekuwa wavumilivu lakini pia wamekuwa sehemu ya kutoa ushirikiano ili kuweza kutatua matatizo ya migogoro ambayo ipo kwenye mipaka. Sisi katika Jimbo letu la Ushetu tumepakana na Hifadhi ya Kigosi Moyowosi lakini pia tuna hifadhi za misitu nyingi kwenye Kata za Ulowa, Ubagwe, Ulewe, Nyankende, Idahina na Igomanoni. Kote huko tunapakana na misitu lakini wananchi hawa wamekuwa na utayari wa kushirikiana ili tuhakikishe kwamba uhifadhi unaendelea lakini pia mifugo yetu inapata sehemu ya malisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakubaliana kwamba sekta hii ya maliasili na utalii imetoa mchango mkubwa sana kwenye Taifa letu. Utashuhudia kwamba kuna ajira imepatikana maeneo mbalimbali ya moja kwa moja na ile ambayo ni indirect. Pia imechangia kama wachangiaji wengine walivyosema katika pato la Taifa, fedha za kigeni tumezipata lakini mchango mkubwa umekwenda katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Jambo lingine pia uhifadhi wetu umeipa heshima nchi yetu, niipongeze sana Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini utaona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumza pia kwamba uko mchango mkubwa kwenye nishati. Asilimia 90 ya nishati imetokana na rasilimali zetu hasa hasa za kwenye misitu. Pia kumekuwa na 75% kwa mujibu wa taarifa ya Mheshimiwa Waziri imetupa faida ya kupata vifaa vya ujenzi. Kwa hiyo, utaona kabisa sekta hii ni muhimu lakini ni lazima kuhakikisha kwamba kunakuwa na uhifadhi lakini pia kutokuwa na migogoro ambayo inatusumbua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alivyoanza kutoa hotuba yake aliturejesha kwenye Ibara ya 27 ya Katiba lakini napenda nimshauri Mheshimiwa Waziri ajaribu kuiangalia Ibara ya 24 kwa madhumuni ya kuziangalia sheria zetu. Hizi sheria zetu ambazo zinatoa fursa ya uhifadhi wa misitu yetu zinahitajika ziletwe katika Bunge lako kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho. Kwa sababu ukiiangalia Ibara ya 24, naomba kwa ruksa yako niisome kwa haraka, inazungumza juu ya haki ya kumiliki mali, inasema kwamba:-
“(1) Kila mtu anayo haki ya kumiliki mali, na haki ya hifadhi ya mali yake aliyonayo kwa mujibu wa sheria.
(2) Bila kuathiri masharti ya Ibara ndogo ya (1), ni marufuku kwa mtu yeyote kunyang’anywa mali yake kwa madhumuni ya kuitaifisha au madhumuni mengineyo bila idhini ya sheria ambayo inaweka masharti ya kutoa fidia inayostahili”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo yetu tumekuwa na utaifishaji wa mifugo, sasa nashauri sheria hizi zije hapa tuzitazame. Sheria hizi zimepitwa na muda kwa sababu ukiangalia hata zile sheria ambazo zinatoa uhifadhi katika maeneo kama ya TANAPA ziko faini ndogo sana. Nilikuwa nafikiria kwamba tufanye marekebisho lakini pia itupe nafasi sisi wananchi, kama Mheshimiwa Waziri alivyozungumza katika hii Ibara ya pili, anapozungumza juu ya uhifadhi, nani ahifadhi na hizi rasilimali ni za nani, ni zetu sisi sote. Kwa hiyo, lazima tushiriki pia kuhifadhi na kulinda hizi rasilimali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri afanye mapitio ili tu tupate sheria ambazo na sisi wananchi kwa kupitia vikundi vyetu kama wakati mwingine nilivyoshauri hapa tuweze kutoa nafasi kwa wananchi kupitia vikundi vyetu na uongozi wa mila kuweza kupeana faini kidogo kidogo za kila siku ili kuhakikisha kwamba uhifadhi unakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia katika migogoro hii ambayo imekuwepo, chanzo chake ni nini? Ni ukweli Mheshimiwa Waziri akubaliane na mimi kwamba siku za nyuma tumekuwa na utaratibu kwamba wale wahifadhi walikuwa kwanza hawatoshi lakini pia wamekuwa wakitumika katika kuhifadhi watu ambao walikuwa wanawachukua kwa muda ambao sasa kutokana na kutokuwa na nidhamu tulichochea sana wananchi wetu kuingiza mifugo katika hifadhi. Matokeo yake ilizoeleka kama ni jambo la kawaida kwa mwananchi kupeleka mifugo yake katika hizi hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo kadhaa napenda kushauri. La kwanza Mheshimiwa Waziri lazima tuwe na dhamira ya kweli kwa upande wa Serikali na kwa upande wa wananchi na Waheshimiwa Wabunge ya kutatua hii migogoro, lazima tudhamirie kuliondoa hili suala. Tukidhamiria tutapata nafasi ya kurejesha yale mahusiano ambayo yalianza kupotea ili tushirikiane kwa pamoja kuona kwamba uelewa wa uhifashi unapanuka lakini pia tunashiriki kuweza kuhifadhi maeneo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko pengo la uelewa ambalo nimwombe Mheshimiwa Waziri na timu yake wajipange vizuri ili tuendelee kuwaelimisha wananchi kwa kuweka vile vikundi ambavyo vimetajwa na sheria kwa ajili ya kushiriki katika uhifadhi, kwa pamoja tatizo hili tutaweza kuliondoa. Pia bajeti ya Mheshimiwa Waziri haitoshi ili kuhakikisha mafunzo yanatolewa na vikundi vinasaidiwa ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la wafanyakazi hawa kwa ajili ya doria hawatoshi. Mheshimiwa Waziri litazame suala hili ili tupate watu wenye weledi ili tuweze kwenda vizuri. Pia liko jambo ambalo nafikiria kwamba lazima tuwe na sheria ndondogo kwa upande wetu wa uhifadhi ili tuweze kusaidia kama walivyofanya wenzetu upande wa TANAPA na maeneo ya kwetu iwe hivyo ili tuweze kupiga hatua vyema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najaribu kuangalia taarifa hizi za bajeti katika kipindi hiki cha miaka miwili, mitatu, utaona uharibifu kwa mwaka ni hekta 372,000 lakini kwa mwaka tunapanda miti 95,000 na tunasema ikifikia 2030 tutakuwa angalau tumeweza kuwa na misitu ya kutosha, haiwezekani kwa sababu uharibifu huu ni mkubwa kuliko namna ambavyo tunaweza kufanya hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia gharama za kupanda miti, miche ya miti ina bei kubwa sana Mheshimiwa Waziri aangalie eneo hili kwani wananchi wetu wakipata miche ya miti watasaidia kupanda miti mingi ili tuweze kurejesha huu uharibifu. Kwa hiyo, ukiangalia uwiano wa uharibifu na namna ambavyo tunarejeshea misitu utaona kabisa haiwezekani kuhakikisha kwamba kweli hii maliasili inabaki vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi tumeyazungumza kwenye mifugo, lakini tumesahau kuna eneo lingine ambalo pia linaharibu misitu yetu. Utaona kabisa kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba mkaa tani milioni 1.7 inaingia mjini, asilimia 50 inaingia Dar es Salaam, inatoka maeneo ya pembezoni kuja mjini. Eneo hii ni muhimu sana tuliangalie vinginevyo tutaona kwamba labda mifugo ndiyo inaharibu misitu hii, lakini bado nishati ni sehemu kubwa ya uharibu wa misitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aje na mkakati mzuri wa kuhakikisha kwamba tunaweza kushikiriana na upande mwingine wa nishati mbadala ili kuhakikisha kwamba hii retention ya misitu inakwenda vizuri. Suala la uhifadhi shirikishi ni muhimu sana, lazima tushirikiane na wananchi ili kuhakikisha kwamba misitu yetu inakaa vizuri. Twende sambamba na Wizara zingine kuhakikisha wananchi wetu tunawajengea kipato cha kutosha ili ule ushawishi wa kuharibu na kutumia rasilimali zetu uweze kupungua ili misitu yetu iweze kwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze juu ya utafiti na sensa ya wanyamapori. Nimejaribu kuangalia ripoti mbalimbali naona kwamba kulikuwa kuna sample tu ya sensa kwa kuangalia namna ambavyo wanyama wamepungua, kama tembo wamepungua sana...
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu nzima ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuja na mpango ambao unatekeleza ule mpango wa miaka mitano, Mpango wa Maendeleo endelevu na ilani ya CCM. Nipongeze mambo yafuatayo ambayo ni makusanyo yameongezeka na udhibiti wa matumizi umeongezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iangalie kwa makini changamoto zifuatazo:-
Ukusanyaji wa kodi wenye ufanisi na matatizo ya ukusanyaji kwa maofisa na walipa kodi. Uwekezaji sekta binafsi kumudu ushindani wa bidhaa nje unaotokana na “application ya VAT; cash flow management, mzunguko wa fedha (money supply), ukuaji wa uchumi na hali halisi ya maisha, kupeleka fedha za bajeti zilizotengwa na kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri, Serikali iendelee kupanua wigo wa ukusanyaji, mkazo uwe pia kwenye makato yasiyo na kodi (non-tax revenue) hususan taasisi zilizo chini ya TRA. Tuangalie namna kodi (VAT) itakavyowalinda sekta binafsi, tuangalie mnyororo wa huduma, mfano tuwezeshe kilimo chenye tija, kilimo kitoe malighafi za viwanda tujenge viwanda ambavyo ni soko la viwanda vyetu. Kilimo na viwanda vitainua uchumi na kuleta ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie vizuri utekelezaji accounting framework ya “accrual basis of accounting ili tuweze kuwa na cash ya kutosha mwanzoni mwa mwaka miradi isisimame mwanzoni mwa mwaka. Uwepo uhakiki wa data “data integrity” ili consumer price index” ijengwe kwa kuzingatia mtawanyiko wa masoko.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii itawasaidia menejimenti ya real economy na Nominal economy ili kuondoa dhana ya ukuaji uchumi na hali halisi. Program based on budgeting inayolenga kuanza na Wizara nane itayarishwe kwa makini kwani inahitaji taarifa nyingi, inataja kuwa na “activity” nyingi, ngumu sana kuainisha shughuli (activity) na matokeo lengwa/malengo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono mpango huu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutoa shukrani kwa Hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na naunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Waziri Mkuu kwa umakini wake na upendo mkubwa alionao anapotekeleza majukumu yake na unapompelekea jambo lolote yuko tayari kulishughulikia mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba tena Waziri Mkuu atusaidie kutatua mgogoro unaofukuta juu ya umiliki halali wa majengo ya Halmashauri ya Ushetu yaliyoko Kahama Mjini ambayo bila kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu, Serikali ya Mkoa imeagiza yamilikiwe na Halmashauri
ya Mji wa Kahama na kunyima fursa Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu kupanua wigo wa mapato yake na kuongeza huduma bora kwa wananchi. Vilevile inaiweka katika hatari ngumu kisiasa eneo letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la maji ya mradi wa Ziwa Viktoria; naishauri Serikali kuangalia impact ya upelekaji wa maji yaani kufanya mapitio kiasi gani au idadi gani ya watu wanasambaziwa maji kuliko kuridhika na dhana pekee ya kuwa maji yamefika Makao Makuu ya Wilaya
hali maji hayajawafikia wananchi walio wengi. Mfano; maji ya Ziwa Viktoria yamefika katika Makao Makuu ya Wilaya na wananchi wengi hawajasambaziwa maji hayo ikiwemo eneo lote la Jimbo la Ushetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie suala la kutusambazia maji eneo la Jimbo la Ushetu sehemu ambayo ina shida kubwa ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo naiomba Serikali iweke mkazo na kusimamia na kuleta tija katika uzalishaji:-
(i) Suala la pembejeo ipatikane ya kutosha, ipatikane mapema (ii) Benki ya Kilimo iwezeshwe mtaji wa kutosha na isimamiwe vizuri ili iweze kutekeleza majukumu yake hususani:-
(a) Kutoa mikopo kwa wakulima.
(b) Kufanya utafiti wa kifedha na kiuchumi.
(c) Kutoa elimu kwa wakulima.
(d) Kuwajengea uwezo vijana na kuwawezesha kwenye miradi ya kilimo.
(e) Kuratibu utoaji mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la madini naomba Serikali iwasaidie wachimbaji wadogo wadogo wapate maeneo yao ya uchimbaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano katika eneo la Mwabomba Jimbo la Ushetu kuna hali ya sintofahamu wachimbaji wadogowadogo waliopo watakwenda wapi kufuatia eneo hilo kupewa mwekezaji ambaye anasuasua kuanza shughuli zake wakati huo huo Mheshimiwa Rais wetu
Dkt. Magufuli aliwaahidi wananchi kuwa hawatahamishwa eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate ahadi ya Serikali juu ya hatma ya wachimbaji wadogo wadogo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba ambazo ziko mbele yetu na niaze kwa kuunga mkono kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais kwa nia yake thabiti ya kusaidia wanyonge, namshukuru Waziri Mkuu, sikupata nafasi ya kuchangia kwenye hotuba yake, lakini namshukuru sana kwa kutusikiliza, tunapokuwa na masuala anayashughulikia kwa haraka sana.
Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri, ndugu yangu Mheshimiwa George Simbachawene, Mheshimiwa Jafo na dada yangu Mheshimiwa Kairuki kwa hotuba nzuri. Nimepitia hotuba hizi na jedwali hili ambalo Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI ametuwasilishia hapa, yapo mambo ambayo kwa kweli inaonesha kabisa Wizara imejipanga vizuri, na mimi nimefarijika sana kuona kumbukumbu nzuri ambazo pia zitatusaidia katika kutekeleza majukumu yetu. Kwa hiyo, nashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nianze kutoa mchango wangu kwa kuzungumza juu ya uratibu, hususan najikita kwenye hii Wizara ya TAMISEMI, kwamba Wizara hii inayo majukumu mengi lakini napenda tu nipate nafasi hii niweze kuomba sana katika kuratibu maeneo mbalimbali ambayo pia
yanasimamiwa na sekta nyingine kwa mfano kwenye kilimo waweze kuangalia vizuri ili watusaidie wananchi wetu. Sisi tunaotoka majimbo ambayo pia ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo, waweze kutusaidia. Kwa sababu najua wanasimamia upande wa pembejeo, tumekuwa na shida kubwa, tunahitaji uratibu uwe wa mapema ili wananchi wetu wapate pembejeo mapema tuweze kuongeza uzalishaji.
Mheshimiwa Spika, yapo maeneo mengine ambayo yanahitaji kufanya utafiti. Tunaona kuna suala hili la kuwa na akiba ya chakula, imefika wakati sasa Wizara ijaribu kuangalia kama tunaweza kupata fursa pia ya kuhifadhi chakula, tuwe na maghala kwenye upande wa Serikali za
Mitaa kwa maana ya Halmashauri zetu ili tuwe na akiba lakini pia tunaweza kufanya biashara kupitia zoezi hili la kuhifadhi chakula. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia napenda kushauri kuhusu usimamizi wa mikopo kwa wakulima wetu kwa sababu Wizara hii kwa idara ambazo zipo kwenye Halmashauri zetu, ikisimama vizuri tutaweza kuwasaidia wananchi. Kwa sababu utaweza kuona kwamba mikopo ambayo inakwenda kwa wakulima kwa mfano wa zao la tumbaku, utaona ile mikopo na mikataba inayotolewa na vyombo vyetu ambavyo vinakopesha wananchi kumekuwa na biashara ndani yake ambayo inawaumiza sana wakulima.
Mheshimiwa Spika, kwa mfano mikataba ambayo inakuwa imetengenezwa kwa kufuata fedha za kigeni, kwamba wakati wa kukopa unapopewa pesa kwenye kubadilisha pesa kutoka dola kwenda shilingi, pale kuna gharama ambazo zinakuwepo na wakati wa malipo
kadhalika kunakuwa kuna gharama ambazo mwisho wa safari wakulima wetu wanapata gharama kubwa kutokana na mikopo hii.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda nishauri kwenye kuratibu, tuimarishe maeneo ambayo kwa upande wa idara ambazo zinasimamia wakulima hawa hususan hawa wa tumbaku tuweze kuona kwamba mikataba yao pia inakuwa mizuri kwa wakulima.
Mheshimiwa Spika, nilitaka nizungumze juu ya uongezaji wa makusanyo katika Halmashauri zetu. Kwa maana hiyo, naiomba Wizara hii ya TAMISEMI iweze kutusaidia pale ambapo kwa upande wetu sisi kama Halmashauri tunavyokuwa na mipango ya kuwekeza ili tuweze kupanua
makusanyo katika maeneo yetu, kwa sababu hapa kuna tatizo kwamba tunavyotaka angalau tu-cross border, tuweze kufanya uwekezaji kwenye maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI anajua kwamba sisi tuna dhamira kubwa ya kutokutegemea ushuru tu wa mazao, tunapenda pia twende tufanye uwekezaji ili Halmashauri zetu ziweze kuongeza mapato.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu Wizara hii iweze kufanya coordination nzuri ili tutakapofika kwenye maeneo ambayo tunataka kupanua vyanzo, basi watusupport ili tuweze kuongeza makusanyo. Kuongezeka kwa makusanyo ina maana huduma kwa wananchi wetu itakuwa inaongezeka.
Mheshimiwa Spika, nataka nizungumze juu ya udhibiti wa ndani (internal controls), lakini nataka nijikite kwenye maeneo mawili; kuimarisha hili eneo la Wakaguzi wa Ndani na upande mwingine nitazungumza juu ya Kamati za Ukaguzi ambazo hazijafanya vizuri, zimeleteleza kutokuwa na udhibiti mzuri katika makusanyo na katika matumizi. Kwa hiyo, nafikiria nizungumze maeneo haya mawili.
Mheshimiwa Spika, nimeona kwamba katika maeneo yetu upande wa Wakaguzi wa Ndani bado tuna matatizo makubwa. Kwanza Wakaguzi hawa wa Ndani ni wachache sana, hawawezi kumudu kuwa na mawanda ya kutosha (scope) ili ule ushauri wao uweze kusaidia Halmashauri yetu.
Mheshimiwa Spika, nafikiri Wizara hii itazame sana eneo hili, kwa sababu ukiangalia Wakaguzi wa Ndani, hawana hata ule mpango. Sisi tunao Wakaguzi wawili; hawana hata ule mpango ambao utaonesha kwamba wamejipanga vizuri ili kuweza kupitia maeneo ya kutosha
na kuweza kushauri katika Halmashauri ili tuweze kufanya vyema.
Mheshimiwa Spika, utakuta Wakaguzi hawana hata ule ujuzi wa kutosha kuweza kuangalia labda kuwa na uwezo kwenye mifumo hii, ujuzi wa TEHAMA uko mdogo, hawawezi ku-access information kwenye EPICA, Lawson, kwenye PLANREP, kwa hiyo, utaona kwamba hili ni tatizo. Hawa Wakaguzi wa Ndani waongezwe lakini pia waweze kuwa na weledi wa kutosha waweze kuzisaidia Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Spika, utakuja kuona kwamba hata bajeti, nilipokuwa nikipitia bajeti ya kwenye Halmashauri yangu, niliwauliza Wakaguzi wa Ndani kama fedha zinatosha.
Kwa hiyo, unaona kwamba hata pesa wanazopangiwa ni kidogo sana kuweza kumudu majukumu yao na pia wana shida ya vifaa, hawana kompyuta, hawana magari ya kutembelea maeneo mbalimbali, maeneo ya kwetu ambayo ni makubwa sana. Kwa hiyo, utaona kwamba ule mchango wao ni mdogo sana ambao kimsingi kama maeneo haya tutayaboresha, watatuwezesha pia Maafisa Masuhuli kufanya kazi zao vizuri kwa sababu watapata ushauri na kwa mapema zaidi.
Mheshimiwa Spika, hili eneo la Kamati za Ukaguzi utaona Kamati ya Ukaguzi ni muhimu sana kuwepo katika Halmashauri yetu, lakini bado hatujaziwekea msimamo mkubwa kuweza kuhakikisha kwamba Kamati hizi zinafanya kazi na kusaidia mambo mengi sana.
Kwa hiyo, utaona eneo hili ni muhimu sana, TAMISEMI ilitazame ili waweze kusaidia. Hizi Kamati zitamwezesha Afisa Masuhuli kutimiza wajibu wake kwa sababu ataweza kumshauri vizuri majukumu yake ya kiuongozi, zitasaidia sana kama zitaimarishwa. Pia tutapata ufanisi katika hiki kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kwa sababu hii Kamati ya Ukaguzi inamsimamia kwa ukaribu sana huyu Mkaguzi wa Ndani. Kwa hiyo, nafikiri eneo hili pia tuweze kulitazama.Mheshimiwa Spika, nizungumzie juu ya maboma.
Tunayo maboma mengi sana ambayo wananchi wametumia nguvu nyingi sana kujenga, katika hili TAMISEMI watusaidie sana kuyakamilisha haya maboma. Nilikuwa najaribu kuangalia kwenye haya majedwali, utaona kabisa kwamba kuna upungufu sana. Kwa mfano, nilikuwa najaribu kutazama nikaona upungufu wa madarasa katika shule za msingi na sekondari. Kuna upungufu mkubwa sana ukiangalia majedwali haya, lakini wananchi wamejitolea vya kutosha; yako maboma mengi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ninazo nyumba 170 ikiwemo madarasa, zahanati, majengo ya utawala, nyumba za walimu, nyumba za wafanyakazi wa afya 170 ambazo zinasubiria kukamilishwa. Hii idadi ni kubwa sana, bila Serikali kutusaidia Halmashauri peke yake haiwezi. Pia yapo majengo 117 ambayo yako kwenye hatua mbalimbali; hatua ya msingi, hatua ya madirisha na hatua ya lenter Serikali naomba
itusaidie sana ili tuweze kupunguza huu upungufu ambao upo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana TAMISEMI watazame eneo hili kwani wananchi wameweka nguvu nyingi, watapata moyo sana kama Serikali itatusaidia kuweza kukamilisha masuala haya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine, nilipokuwa nikipitia hili jedwali, nimeona kuna shule zimesahaulika. Nashukuru kwamba tumepata walimu wa sayansi wachache, lakini ninaamini kwamba sisi katika Halmashauri ya Ushetu tunayo shule ya high school inaitwa Dakama secondary school, haikupangiwa walimu na ina upungufu; haina walimu wa sayansi. Walimu wa physics, tunaye mmoja ambaye ndio Mkuu wa Shule, anafundisha kuanzia form one mpaka form six.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Hatuna mwalimu wa biology! Sasa naomba Wizara itazame ili tuweze kusaidia hawa watoto. Isipokuwa nimegundua kwamba ilisahaulika kwa sababu, ukiangalia hata katika majedwali kwenye mgao wa fedha za usimamizi wa mitihani, hatukupangiwa high school. Kwa hiyo, naamini kwamba shule hii ilisahaulika.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba uitazame hii shule ili tuokoe hawa watoto waweze kupata huduma na tuweze kufanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kumwomba Mheshimiwa Waziri TAMISEMI, kusaidiwa madaraja matatu…
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika hii hotuba muhimu. Kwa kweli kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru sana Serikali; naishukuru sana Wizara hii, naungana na wasemaji waliotangulia, ukiangalia hotuba hii kwa kweli imeanza kutupa suluhisho la matatizo katika kilimo. Mambo mengi ambayo yameonekana kwenye hotuba hii nawiwa kutoa shukrani sana kwa Mheshimiwa Waziri Tizeba na timu yake. Naona sasa kwamba iko dhamira ya kusaidia wakulima tuweze kuinua uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru pia wananchi wa Ushetu kwa kutoa mchango mkubwa sana katika kilimo. Kilimo chetu katika eneo letu ndiyo kinatupa pia mapato ya kutosha katika Halmashauri kupitia mazao ya biashara; pamba na tumbaku, tunaweza kuendesha vizuri na kutoa huduma vizuri katika Halmashauri yetu. Kwa hiyo, nawapongeza sana wananchi pia kwa uvumilivu. Tumekuwa na shida kubwa, katika msimu uliopita hatukupata kabisa pembejeo kwa mazao mengine, lakini pamoja na hayo naona tulikuwa tumeweka nguvu kubwa sana kuhakikisha kwamba tunaweza kuzalisha chakula na mazao mengine ya biashara vya kutosha. Kwa hiyo, nawapongeza sana wananchi wa Ushetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo ni uti wa mgongo. Utaona katika hotuba hii, Mheshimiwa Waziri amerejea kutukumbusha kwamba kilimo kinachangia sehemu kubwa la pato la Taifa, kinaajiri watu wengi. Sisi tuseme kwa upande wa kwetu Ushetu, kilimo ndiyo hicho ambacho tunakitegemea kiweze kututoa katika huu umaskini. Kwa sababu mimi naweza kusema kwamba asilimia mia moja ya wananchi wa Ushetu tunajihusisha katika kilimo. Iwe ni Mbunge, nalima; Diwani, analima; awe ni mfanyabishara, analima. Kwa hiyo, watu wote wanajishughulisha na shughuli za kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaona kabisa sisi ni wadau wakubwa na tunahitaji sana hii Serikali itusaidie ili tuweze kusonga mbele zaidi. Kwetu hata wanafunzi pia wana mashamba. Kwa wale wenzangu wanajua jilaba, kwamba tuna mashamba madogo madogo ya wanafunzi. Hata watoto wadogo wa shule wana part time ya kulima, wanakuwa na mashamba. Kwa maana hiyo, tunaona uko umuhimu sana kwamba tunawazoesha watoto kwa nia ya kuona kwamba wanathamini hiki kilimo kweli na ni uti wa mgongo wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo hapa nataka niyaseme tu kwa ufupi sana. Kwanza naiomba sana Serikali kupitia Wizara hii, iweke dhamira ya kweli kuweza kuhakikisha kwamba haya ambayo yapo kwenye hotuba yanatekelezwa ili yaweze kutusaidia. Kwa sababu utaona kabisa kwamba ni muhimu tuzalishe ili tuwe na chakula cha kutosha na kwa kweli tutakuwa tunaweza kuinua uchumi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri sana Serikali pia iangalie na kuchambua, kuna mambo ambayo tunayaona kwenye ripoti. Kwa sababu nilikuwa nikiangalia taarifa ya BOT ya Mwezi Machi, 2017, naona ile trend ya uzalishaji mazao, bei na mauzo ya nje imekuwa ikishuka. Sasa naishauri tu Serikali ifanyie kazi, ichambue vya kutosha ili baadaye tuweze kupata suluhisho la kuona kwa nini wakati wote uzalishaji, bei na mauzo yanaendelea kushuka?

Mheshimiwa Naibu Spika, naweza kutolea mfano katika zao la tumbaku ambalo sisi tunalizalisha kwa wingi. Nimeona mauzo ya tumbaku yamekuwa yakishuka sana. Kuanzia mwaka 2013 tuliweza kuwa na mauzo ya dola milioni
7.3 lakini mwaka uliofuatia (2015) tuliweza kufikia dola milioni 41.2; lakini utaona kabisa mwaka 2017 kuna dola 9.4, tulishuka sana. Sasa na mazao mengine ya kahawa, pamba, katani, korosho na karafuu, utaona kuanzia mwaka 2013 mpaka 2017 tumekuwa tukiendelea kushuka, lakini pia ule uzalishaji kwa ujumla utaona nao umeshuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasoma nikaona kwamba mwaka 2013 pia tulikuwa na tani chache ambazo tulikuwa tumezalisha, lakini mwaka 2015 kulikuwa na uzalishaji mkubwa wa zao hili la tumbaku lakini mwaka 2017 pia tumeshuka karibu nusu. Lazima tuseme kwa nini tunashuka hivyo? Kwa hiyo, nafikiri hizi data zinazopatikana ni vizuri Serikali ikazifanyia kazi ili tuweze kuinua uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kilimo ni muhimu kwa sababu nilikuwa naangalia uwiano tu wa mazao ambayo tuliuza nje, ukilinganisha na maeneo mengine ambayo tulikuwa tumejipatia kipato, tumesafirisha madini na bidhaa nyingine za plastiki na kadhalika. Sasa kwenye kilimo, mifugo na uvuvi tulikuwa tumepata kati ya asilimia 59 hadi 64 ndiyo mchango wake. Kwa hiyo, unaona kabisa kwenye eneo hili ni muhimu sana kulitazama ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwetu tunapata mvua mapema kuanzia Septemba. Kwa hiyo, niisihi tu Serikali yangu kupitia Wizara hii kwamba suala la pembejeo liwekewe umuhimu wa hali ya juu kwamba ikifika mwezi wa Tisa tuweze kupata hizi pembejeo mapema kama mbolea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeze sana Serikali kwa kuja na utaratibu huu wa kuagiza hii mbolea kwa pamoja kwa sababu ilikuwa ni tatizo kubwa sana. Hili zoezi la mbolea likisimamiwa vizuri kwa kuzingatia kwamba wananchi katika baadhi ya Kata zetu zimekuwa ni model, tunazalisha kuanzia gunia 25 hadi 30 kwa ekari endapo tunalima kwa wakati na kutumia pembejeo kwa usahihi. Ziko Kata ambazo zimeonesha mfano, kama Kata ya Kinamapula, Kata ya Ubagwe, Kata ya Ulewe, zimeweza kuzalisha hadi magunia 30 kwa ekari.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa mwaka uliopita 2016 hatukupata pembejeo hizi kabisa kwamba wananchi wamekuwa na manung’uniko kwa kukosa mbolea. Kwa hiyo, naiomba tu Serikali kwa kipindi hiki kinachokuja na kwa vile tumeendelea kuwaahidi wananchi kupitia vikao vyetu kwamba Serikali inajipanga katika utaratibu mzuri, ambao ndiyo huu sasa Wizara imekuja nao, kuhakikisha wananchi wapate hii mbolea ya kutosha lakini waipate kwa wakati ili sasa twende tukazalishe; na tuweze kuhakikisha kwamba hili suala la njaa linaondoka kabisa na uchumi unakwenda juu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine Mheshimiwa Waziri atusaidie; kwa vile tunazalisha chakula cha kutosha na kumekuwa na shida sana ya soko la mazao ya chakula hapo mwanzoni tunapoanza kuvuna, kama inawezekana kupitia Halmashauri zetu Mheshimwia Waziri asaidie tupate maghala ya Halmashauri ili tuweze kuhifadhi chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo wananchi wanahitaji tena kupata fedha kwa haraka kwa ajili ya maandilizi ya kilimo, waweze kuuza na kupata fedha. Wakati huo tutakuwa tunahifadhi chakula kwa ajili ya matumizi ya Taifa kwa ujumla na wananchi wanapata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana tuliangalie hili, kwa sababu kama chakula kinazalishwa kwa wingi na wananchi wanategemea kuweza kupata fedha kutokana na ziada kwa ajili ya kushughulikia mambo yao mbalimbali pamoja na maandalizi ya kilimo kwa msimu unaofuata, tunavyofanya zuio la wananchi kufanya mauzo ya chakula hiki cha ziada, kwa kweli inatuharibia ile trend nzuri ya kwenda kuzalisha kwa wingi msimu mpya. Naomba hii tuitazame. Kwani wengine wanaendesha kilimo kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee na suala la mbegu. Tumeona mkazo mkubwa umekuwa kwenye mbegu chache, zaidi kwa mbegu za mahindi. Kwa mfano, tunaweza kupata mbegu za mahindi kwenye maduka, lakini tumeacha kwenye maeneo mengine kama mbegu za pamba kupata zenye ubora, kupata mbegu za mpunga na zenyewe hatuzipati. Kwa hiyo, nafikiria Serikali iangalie pia zoezi hili la mbegu za kila aina.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia matumizi ya maabara. sisi kwetu Ushetu tumekuwa na maabara ndogo ambazo Serikali imetusaidia, nashukuru sana. Katika Kata ya Mpunze tunacho kituo kwa ajili ya kufanya majaribio ya hizi mbegu, lakini hakijatumika sawasawa. Naomba Serikali iweze kuweka msisitizo ili kama mbegu mara zinapopatikana, basi maabara hizi zianze zenyewe kuotesha ili tuone kama germination rate iko nzuri ili wananchi wanavyonunua hizi mbegu tuwe na uhakika kwamba mbegu hizi hazijachezewa, tumepata mbegu zenye ubora na tuweze kusonga mbele bila wasiwasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana, kama tumekuwa na maabara hizi zitumike, lakini zitupe majibu; nasi tutadakia kwa ajili ya kuelimisha wananchi wetu umuhimu wa kutumia hizi mbegu ambazo ziko bora inavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda nishauri ni kwa kumalizia tu ni kuhusu matumizi ya hizi nyenzo; trekta na power tiller, lakini utaona kwamba mashine hizi zinapatikana mjini tu. Wizara ijipange, ione namna ambavyo itatuwekea vituo angalau kidogo tuwe na sample ya hizi mashine au vitendea kazi. Wananchi wayaone waweze kuhamasika kuweza kutumia haya matrekta.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu kwa sehemu kubwa tunalima sana kwa kutumia maksai. Kwa maana hiyo wananchi wako na utayari sasa wa kurahisisha kilimo chao na sisi baada tu ya mvua kunyesha wiki moja ile ya kwanza tunaweza kukamilisha mashamba yetu. Wananchi wana speed kubwa, hawataki kupoteza wakati pale mvua za mwanzo zinavyoanza kunyesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasi maeneo yetu Mheshimiwa Waziri atazame ili haya matrekta ambayo yako kwenye mpango wa kuzalisha yatakapokuwa tayari, basi yasogee katika maeneo yetu ya uzalishaji ili pia wananchi waweze kupata hamasa. Tunao uwezo wa kununua matrekta ili tuweze kuzalisha kwa wingi zaidi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hii hoja muhimu ya Wizara ya Fedha na Mipango. Niungane na wenzangu niwatakie wote waliofunga wawe na funga yenye heri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza hii Wizara, nimpongeze Waziri Mpango, Naibu wake, Watendaji wote na Taasisi nyingi ambazo ziko chini ya Wizara hii kwa mafaniko makubwa. Kwa sababu ukiangalia parameter za uchumi, utaona kwamba tunaenda vizuri, bila kuwa na coordination nzuri ya Wizara hii isingewezekana. Kwa hiyo nawapongeza sana wote. Niipongeze pia Mamlaka ya Mapato kwa makusanyo, napongeza pia usimamizi kwenye idara ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali. Kipindi hiki tumepokea ripoti nyingi sana, ukiangalia hata kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ripoti zaidi ya 600 kwenye majumuisho yake siyo kazi ndogo, kwa hiyo nitumie fursa hii kuwapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze jambo moja kuhusu Wizara hii ya Fedha inayo mchango mkubwa sana kwenye maendeleo ya kilimo. Nataka nijikite kwenye eneo hilo. Nitapenda nizungumzie taasisi mbili kwa maana ya hii Benki ya Kilimo na kampuni ya mbolea. Kwa sababu kilimo kwa ujumla wake kina mchango mkubwa sana kwenye ukuaji wa uchumi, kwa hiyo nafikiri nizungumzie haya maeneo mawili ili nione kwa namna gani naweza kushauri Serikali kupitia Wizara hii muhimu itusaidie wakulima wa Tanzania, wakulima wa Ushetu na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona kabisa katika kilimo kweli tutapata chakula, biashara zitashamiri lakini pia ni sehemu kubwa ya kutoa mchango wa mapato yasiyo ya kodi (non tax revenue) inatoka katika eneo hili la kilimo kama Wizara hii itasukuma vizuri na kilimo chetu kiwe chenye tija, ili tuweze kuondokana na kilimo hiki kwa ajili ya kujikimu, ili tuweze kwenda kwenye kilimo cha kibiashara na mapinduzi ya kilimo hasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona yako mambo mengi mazuri ambayo kama Serikali imeyaandaa yanahitaji sasa msukumo wa kipekee ili kuona mchango wake unakuwa mkubwa. Kilimo hiki kitachangia ajira, kilimo hiki pia kitachangia malighafi ya viwanda na katika hali ya ukuaji wa uchumi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukijaribu kuangalia hata kwenye mfumuko wa bei tumekwenda vizuri sana tuko kwenye digiti moja kama Mheshimiwa Waziri alivyokuwa akizungumza, tuko kwenye karibu asilimia sita, lakini ukiiona hii kwenye upande wa chakula bado mfumuko wa bei siyo mzuri. Tungekuwa na indicator kwa ujumla wake ingeshuka sana kama eneo hili la kilimo litakwenda vizuri. Kwa mfano, sasa hivi kwenye chakula peke yake mfumuko wake wa bei uko kwenye asilimia 11 hivi, ukisoma kwenye tafiti mbalimbali. Kwa hiyo utaona kabisa kwamba tunavyokwenda kuiona inflation kwa ujumla wake kwenye asilimia sita lakini upande wa kilimo imejaribu kutupandisha juu, tungeweza kushuka chini zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko juhudi mbalimbali Serikali ikiwa inafanya ili kuhakikisha kwamba kiwango cha uzalishaji kinakuwa kina tija kwenye kilimo. Kwamba tuende kwenye ukulima ambao unatumia pembejeo za kutosha pia teknolojia ya kisasa, bado kuna matumizi madogo kwenye upande wa umwagiliaji. Sasa bila Wizara hii kuweka nguvu yake na kuwezesha vile vyombo ambavyo kimsingi vinasaidia sio moja kwa moja inaweza ikasaidia pia kwenda kupandisha uzalishaji kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji wakulima waende kulima kisasa, wawe na mashamba makubwa, wawe na mitaji ya kilimo, pamoja na kuwa kuna sekta zingine zinasimamiwa na Wizara zingine lakini bila Wizara hii ya Fedha utagundua kabisa kwamba hatuwezi kwenda kuwa na kilimo kikubwa ambacho kitachangia katika ukuaji wa haraka wa uchumi wetu. Kwa hiyo, nafikiri kwamba lazima Serikali kupitia Wizara hii ituangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia hata mikopo inayotoka ina riba kubwa na bado kuna uchache wa maghala ya kuhifadhia chakula, mara nyingi nimekuwa nikizungumza, naona iko haja ya kuwa na tafiti za kutosha ili kwanza tuwe na chakula cha kutosha ili tuende kwa usalama zaidi. Pia tunahitaji kuchakata mazao yetu ili yaweze kuongeza ubora wake hatimaye yatuingizie fedha za kutosha. Kuna madhara mengi pia katika uhifadhi wa mazingira, kwa hiyo uko umuhimu wa Serikali kupitia Wizara hii kutazama sana kwenye eneo hili la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Kilimo imeanzishwa mwaka 2014 lakini bado msukumo na mtaji ni mdogo sana. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aiongelee.

Nimeiona kwenye hotuba yake nzuri hii, katika ukurasa wa 47 ameizungumza lakini kidogo sana. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma, tulipozungumza na benki hii tunaona yako mahitaji ya kuiongezea mtaji. Kwa hiyo, niombe sana Serikali itazame kwa sababu ilikuwa hairidhishi pale ambapo tunaona benki hii imejipanga kutoa mikopo yenye riba ambayo ni nafuu, sasa kama hawana mtaji wanahitaji nao waende kwenye Commercial Bank ili wakakope fedha halafu waje wakopeshe wakulima wetu, haitawezekana hizi rate ambazo wamezionesha kwenye sera yao. Kukopesha mikopo ya bei nafuu haitawezekana kama na wao wanaenda kwenye mabenki mengine yenye riba kubwa kwa sababu mtaji wao bado ni mdogo. Mtaji wao uko kwenye bilioni 60 lakini Serikali ilikuwa imeahidi kusaidia angalau bilioni 100 kila mwaka kwa miaka nane ili benki hii iende kwenye mtaji wa bilioni 800.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona sasa muda umekuwa mwingi bado benki hii haina mtaji wa kutosha. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba sana aitazame benki hii ili mwisho wa safari tuweze kuona kwamba wakulima wetu wananufaika. Utaona kabisa kati ya majukumu mazuri ambayo benki hii tumeipa baada ya kuianzisha inatakiwa iweze kutoa mikopo yenye riba nafuu, itatakiwa ifanye tafiti za kifedha, tafiti za kiuchumi katika sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona kabisa kwamba ukienda kwenye maeneo ya vijiji bado tuna shida hata hii mikopo inayotoka tunaiona ina sura nzuri ya riba ya asilimia 18 lakini effective rate yake kama hatufanyi tafiti za kutosha wakulima wale wanachajiwa kwa mwezi, ukifika mwisho wa safari utaona zile rate zina-attract cost kubwa ambayo ukirudisha ukafanya re-alculation utaona inakwenda mpaka zaidi ya asilimia 30. Kwa hiyo, wakulima wetu wanaumia hawawezi kufanya kilimo ambacho kitaweza kuwapa faida kama hii haitazamwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo benki hii ikiwezeshwa inaweza ikasaidia kuweza kufanya tafiti na kuona kama maeneo yanawapunja sana wananchi iweze kusaidia. Pia itakuwa zoezi zuri la kutoa elimu na kujenga uwezo kwa wakulima, kujenga uwezo kwa ushirika, kujenga uwezo kwenye taasisi zingine za kifedha kama hizi micro- finance hizi zinazokuwepo zinategemea sana chombo kuwe na ambacho itazisaidia ili mwisho wa safari wakulima wetu waweze kunufaika. Kwa hiyo, nafikiri iko haja ya kuiangalia benki hii iweze kupata mtaji ambao utaiwezesha kuweza kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sehemu niliona kwamba kulikuwepo na utaratibu wa benki hii kupata mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Sasa sijui Mheshimiwa Waziri tumefikia wapi? Kwa sababu ilikuwa inatia matumaini angalau wangepata hizi dola milioni 93.5 ambazo tulizungumza kwenye Kamati, kama bilioni 204 angalau ingekuwa nusu ya safari tunaanza kusonga mbele. Sasa tumefikia wapi na huu mchakato wa kuisaidia hii benki kupitia huu mkopo ambao Serikali kupitia Wizara hii ilikuwa imefanya arrangement, napenda tujue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado iko pledge nzuri sana kuelekea mwaka 2020/2021 kwamba tuwe tumefikisha hii benki kuwa na mtaji wa trilioni tatu, ingeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa sana katika hii sekta ya kilimo. Kwa hiyo, nafikiri tuitazame kwa nia ya kuiboresha lakini mwisho wa safari tunavyokwenda kwenye uchumi wa kati tutawasaidia sana wananchi wetu ambao wana utayari sana wa kuzalisha kwa tija ili iweze kuleta mchango mkubwa katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la kampuni ya mbolea. Kampuni ya mbolea imeanzishwa miaka mingi, imeanzishwa mwaka 1968 lakini ilikuwa na shughuli moja tu ya kushughulikia uzalishaji wa pembejeo pamoja na mbolea kule Tanga. Hata hivyo, hapa mbele ya safari tumekuwa na mkwamo, matokeo yake sasa imekuwa ikiendelea kuwa na jukumu moja la kusambaza mbolea. Usimamizi wake haukuwa mzuri kwa sababu mbolea imekuwa ikitufikia huko vijijini ikiwa na gharama kubwa. Nashukuru Wizara ya Kilimo kuja na mpango wa kununua
mbolea kwa pamoja. Bado natazama na chombo hiki kitaingia wapi ili kiweze kusaidia? Kwa sababu chombo hiki kimekuwa na msukosuko mkubwa sana, kina changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Serikali inadaiwa na kampuni hii, lakini pia utaona kwamba, imekuwa ikipata hasara kubwa sana. Mpaka kufikia mwaka 2015 ilikuwa na accumulated losses ya 30 billion, lakini hawa wanahitaji mtaji, walikuwa wanaomba wapewe kama bilioni 27. Sasa haipendezi kuona wanaomba shilingi bilioni 27 wakati wana madeni zaidi ya shilingi bilioni 30. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba aitazame hii taasisi ili iweze pia kutoa mchango wake katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye hoja muhimu hii ya bajeti ya Serikali. Kwanza nianze kumshukuru sana Mungu kwa yote kwa afya na haya yote yanayoendelea, naamini mkono wa Mungu unaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri. Napongeza kwa dhati kabisa na wakati hotuba hii inasomwa, Waheshimiwa Wabunge wengi tulishangilia na yale tuliyokuwa tunayashangilia, naipongeza pia Kamati kwamba imeyazungumza. Sehemu ya tano ukisoma utaona namna Kamati imejaribu kuchambua na kuweka kielelezo namna bajeti hii ilivyoweza kukidhi mambo kadha wa kadha. Hii ni pamoja na kuiangalia hii sura ya bajeti. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niseme kwamba unaweza ukaangalia mafanikio ya bajeti hii na hususani bajeti iliyopita kwa kuangalia yale matokeo (outcomes) kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo, lazima nishukuru sana kwa sababu Jimbo la kwetu ni jipya, Halmashauri ya kwetu ni mpya; hivi sasa tunaendelea kujenga Ofisi kwa kasi; fedha tunazo; tumejenga mashule; kuna maeneo ya maji, tunaendelea kupata huduma za maji na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo mengi siwezi kuyasema yote, nashukuru kwamba hii hotuba ni nzuri kwa sababu ukiangalia bajeti zilizopita ukilinganisha na bajeti hii, utakubaliana nami kwamba kwa kweli hii ni hatua nzuri. Nami naipongeza Serikali iendelee na mwendo huu, tutafika mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nizungumze hili suala muhimu la madini. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa sababu tulikuwa na kiu ya kuyaona mengi na yako mengi ambayo pia yanakwenda kugusa Halmashauri zetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu kama ambavyo nilisema wakati uliopita nilipokuwa nachangia hapa, kwamba ile dhamira nzuri ya Mheshimiwa Rais ndiyo hasa itaweza kuleta msukumo huku chini ili tuweze kufika pale tunapotaka kwenda. Nina uhakika tunakwenda kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najaribu kuangalia baadhi ya figures za report hizi zilizotoka, nikawa najaribu kuona sisi kwenye Halmashauri zetu za Kahama tukiwa na Majimbo matatu ya Msalala, Kahama Mjini na Ushetu, utaona hapa service levy ambayo nikiitaja utajua tulikuwa tumepoteza mapato mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia kwenye dhahabu peke yake kwa report hii, kwa kile kiwango cha chini cha upotevu wa mapato, tumepoteza service levy ya shilingi bilioni 324 kwenye dhahabu peke yake; lakini tukawa na shilingi bilioni 549 kwa kiwango cha juu kwenye dhahabu peke yake. Ukiangalia kwenye madini mengine 13 yaliyoorodheshwa na Tume, utaona kabisa tulikuwa tumepoteza yapata kama shilingi bilioni 397 kwa upande wa madini yote na kwa kiwango cha chini; na kiwango cha juu tunakwenda kwenye shilingi bilioni 689. Nazungumza kwa upande wa hili zoezi lililofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kuangalia kwenye upande wa service levy tulizopoteza kwa wale waliotoa huduma kwenye migodi wakiwemo wale waliofanya insurance, wale waliofanya consultation, waliouza mafuta; naomba sasa hapa Mheshimiwa Waziri atusaidie kwa sababu tulikuwa na shida ya kupata information.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaweza kupata financial statement tangu migodi hii ilivyoanza itatusaidia nasi kwenye Halmashauri zetu kuona wale waliotoa huduma kwenye migodi kama tulipoteza. Tulishaanza hilo zoezi kutafuta hizo information. Tunajua kuna kiasi kikubwa ambacho kingeweza kusaidia Halmashauri zetu. Kuna kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uone kabisa kwamba Mheshimiwa Rais ameanza nasi huku tunaendelea kupigana. Hata alipotembelea Shinyanga wakati ule, nakumbuka ndugu yangu Mheshimiwa Kishimba, Mbunge wa Kahama Mjini alizungumza, tumwombe Mheshimiwa Rais atusaidie kwa sababu tunaona tumepoteza service levy nyingi. Kwa hiyo, kwa upande wa Serikali mnaweza kutusaidia ili tuweze kukomboa na kupeleka maendeleo kwa watu wetu. Sura ya Kahama ilivyo, sivyo inavyotakiwa kuwa kwa fedha nyingi ambazo tunatakiwa kuzipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nizungumze kwa ufupi ni kuhusu hizi takwimu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, hata bajeti iliyopita nilikuwa nimeomba kwamba Ofisi ya Takwimu tuisaidie sana iwe na watu wa kutosha, iwe na vifaa vya kutosha ili tuweze kupata data muhimu za kutusaidia kuweza kufanya mambo mbalimbali, kwa sababu ukija kuona hapa, data nyingi ambazo tunazitumia kwenye records zetu za bajeti na kadhalika, nyingi tunatumia ambazo ni wastani, tunatumia average, lakini sasa tukitumia average tunaacha group kubwa la watu nje ya hizo data ambazo tunazipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati mwingine tunahitaji wataalam wasaidie Ofisi yako kwenda kwenye measures nyingine. Waangalie measures of dispersion ili tuweze kuona tunavyozungumza kwamba wastani wa kipato ni shilingi milioni mbili, lakini tumewaacha watu wangapi nje ya msitari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiria kwamba Ofisi hii iboreshwe, itatusaidia pia kuweza kufanya decision nyingi, tuweze kuona pia tuna income gap ya namna gani? Bajeti iliyotangulia, tuliona pia hata Mikoa ambayo iliyokuwa chini ya mstari wa umaskini. Kwa hiyo, nashauri tu Mheshimiwa Waziri, hii Ofisi ni muhimu sana kuiangalia kwa jicho la kipekee itusaidie kupata information za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo suala la kodi kwenye assessment. Nataka nizungumze tu kwa sababu Commissioner naamini anaweza kuwa yuko hapa. Kwa miaka mingi tumechukua hii kwa kutumia band, tunachukua blanket tu kwenye maeneo fulani. Sasa nafikiri tuendelee kufanya analysis ili mlipa kodi alipe fair kodi kulingana na kipato chake. Kwa sababu utakuja kuona kuna maeneo mengi tunatoza kodi kutokana na eneo, hatuendi kutoza kutokana na uhalisi wa mtu anavyopata kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, twende zaidi kuboresha taarifa zetu ili tutoze kwa usahihi. Kwa hiyo, utaona maeneo mengine kwa mfano, kwenye Mji tunasema labda wafanyabiashara wanaofanana kwenye Mji fulani watozwe kiasi hiki kwenye kodi ya mapato. Kwa hiyo, nafikiri twende zaidi ili tuweze kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hili kwenye zoezi la utozaji wa kodi ya majengo, tukisema tunakwenda kumtoza mtu mwenye ghorofa la Sh.50,000/=, lakini mwenye ghorofa kuna mwingine anaweza akawa ametengeneza kwa leisure tu. Kwa mfano, ndugu zangu Wangoni kule nilikuwa nikienda naona wana maghorofa ambayo wameezeka kwa nyasi. Nilikuwa nakwenda Mbinga, nilishuhudia kuna watu wametengeza maghorofa hayo. Kwa hiyo, tuangalie ili tutoze kutokana na thamani. Vile vile wako watu wengine wana nyumba zao wamepangisha; tukitazama vizuri, tutaona kuna watu ambao wanaweza wakatupa kodi nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa sababu ya muda, nataka nizungumzie juu ya sura ya bajeti. Naona kabisa kwamba upande wa madeni hasa deni la Taifa, tuki- manage vizuri hili deni, utaona kabisa kwamba makusanyo yetu ukiwianisha na hali halisi ya matumizi, kidogo kuna uwiano mzuri. Kwa hiyo, tunakusanya shilingi trilioni 19.2 kwenye mapato ya TRA, kwenye non-tax revenue pamoja na Halmashauri, lakini matumizi yake bila kutoa madeni ambayo tunakwenda kulipa, tuko kwenye shilingi trilioni 22. Kwa hiyo, kuna gap kidogo la shilingi trilioni kama 2.9 hivi. Kwa hiyo, tunahitaji ku-manage vizuri hili deni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona sasa hivi tunakwenda kulipa deni lakini utaona tunakopa shilingi trilioni 11 mkopo wa ndani na nje, lakini tunakwenda kulipa shilingi trilioni tisa. Kwa hiyo, hili gap la deni litaendelea kuzidi. Kwa hiyo, naomba tufanye effort kupunguza hili deni ili siku za usoni tukope kidogo, tulipe kidogo ili tuweze kujenga uwezo mkubwa wa kupeleka fedha nyingi kwenye eneo la maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kuzungumzia juu ya upande huu wa nakisi ya bajeti. Nilikuwa najaribu kuangalia hapa kwamba tumepata nakisi ya bajeti ya 3.8 lakini hapa tumezingatia mapato ya mikopo nafuu kutoka nje, tumewianisha na GDP. Tumeacha pia hii mikopo mingine ya ndani na nje yenye masharti ya kibiashara ambayo ukijumlisha na mikopo ya ndani tunakuwa na shilingi trilioni
11. Sasa nikiwianisha na pato la Taifa, tunaona kwamba ule uwezo wetu wa ku-deal na government spending unakuwa uko short kwa asilimia 11.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiria lazima tutazame yote kwamba tuna uwezo wa kukusanya kodi, tuna uwezo wa kukusanya mapato ya ndani mengine yale pamoja na Halmashauri zetu, lakini ule uwezo wa sisi kupata fedha kutoka nje ya makusanyo yetu tunapungukiwa asilimia 11.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri tulitazame kwa sababu tukitazama upande huu wa mapato ya mikopo nafuu kutoka nje pake yake ya shilingi trilioni tatu, nafikiri siyo sahihi kuweza kuiona hii nakisi ya bajeti. Kwa sababu nilikuwa najaribu kuangalia nchi mbalimbali, nimeona Uholanzi wana- shoot kutoka 2.8 hadi 2.5, Marekani wana 3 - 3.5. Ukiona range, iko within lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja hii muhimu na nianze kwa kuunga mkono hoja. Niitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa sbabau naongea kwa mara ya kwanza kutoa ufafanuzi wa baadhi ya mambo yaliyojitokeza namshukuru sana Mungu kwa nafasi hii lakini nimshukuru kipekee Mheshimiwa Rais kunipa nafasi, kuniamini niweze kumsaidia Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru wewe, nimshukuru Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge maalum niishukuru Kamati tumefanyakazi nayo, tumepokea ushauri wa Kamati na wameendelea kutuboresha katika utendaji wa kazi kwahiyo Mheshimiwa Kakoso pamoja na timu ya Kamati nzima nawashukuru sana.

Nitoe shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa sababu mara zote tumepata ushauri wao, tumepata mijadala mbalimbali tukiwa ndani ya Bunge na nje ya Bunge kwa hiyo, Wabunge tunawashukuru ushauri wenu, maneno yenu kwa kiasi kikubwa yametusaidia kufanya shughuli zetu, lakini pia niwashukuru wapiga kura wa Jimbo la Ushetu muda mwingi kabla ya nafasi hii nimekuwa na muda mwingi wa kuwepo Jimboni, lakini sasa wananikosa na niishukuru pia familia yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme kwamba bajeti hii katika sekta ya ujenzi peke yake imechangiwa kwa kuzungumza hapa zaidi ya wachangiaji 95 na zaidi ya wachangiaji 50 wamechangia kwa maandishi. Niseme tu Katibu Mkuu na timu yake wanaendelea kukamilisha kabrasha la majibu kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge mtayapata na mtaona namna Serikali kupitia Wizara hii inavyochukua hatua mbalimbali kuweza kutekeleza na saa nyingine kuona namna mambo ambayo yamefanyika kupitia pia michango ya kwenu kwa hiyo msiwe na wasiwasi mtapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii, niseme tu kwa ufupi sana nilitaka nitoe na ufafanuzi kidogo kwenye hali ya mtandao wa barabara nchini ili angalau tuwe na picha ya pamoja. Ukiisoma sheria yetu ya barabara hasa hasa ile section ya 12 inatoa mchanganuo wa aina za barabara. Sasa nilitaka nizungumze sambamba ili tuone pia jukumu lililopo kwenye Wizara, lakini jukumu pia ambalo lipo kwa upande wa wenzetu TARURA ili tuone tukifanya mchanganuo pale inaweza ikatupa picha kwamba michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge imezungumza juu ya namna TARURA iwezeshwe zaidi ni kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme tu kwamba kwa upande wa barabara kuu, tukizungumza barabara kuu tunazungumza juu ya barabara ambazo zinaunganisha Makao Makuu ya Mikoa lakini pia barabara ambazo zinaunganisha Makao Makuu ya Mikoa pamoja na majiji au inaunga nchi za nje ambapo kwa sasa tuna barabara zenye ukubwa wa zaidi ya kilometa 12,000 hivi. Lakini tukizungumza barabara zile za Mikoa tunazungumza juu ya barabara ambazo zinatoka kwenye Makao Makuu ya Mikoa zinaunga barabaa kuu.

Lakini barabara pia za Makao Makuu ya Wilaya na Makao Makuu ya Mikoa na hizi sasa kwa ukubwa tunazo kilometa yapata zaidi ya 23,000 sasa utaona kwa upande wa barabara kuu sehemu ambazo sasa zina kiwango cha lami ni zaidi ya kilometa 8,000 na zile ambazo ziko kwenye matengenezo na hata Waziri Mkuu akiwasilisha hapa, kilometa zaidi ya 1,700 ziko kwenye hatua mbalimbali. Sasa ukijaribu kupima utaona upande wa barabara kuu karibu sehemu kubwa tunaunganisha na Kamati imetoa ushauri tumeuzingatia na utaona Mikoa michache ambayo harakati zinaendelea katika hatua mbalimbali kuziunganisha ikiwemo maeneo ambayo yamebakia kama barabara kubwa ikitoka Mkiwa ukipita Itigi kwenda Mbeya, iko barabara kubwa ukitoka Morogoro sasa tunajenga Kidatu kwenda Ifakara lakini ukitoka Ifakara - Lupilo - Malinyi - Londo - Kilosa kwa Mpepo tunakwenda kutoka kule Namtumbo na hiyo barabara harakati zinaendelea vizuri. Kwa hiyo, ziko barabara zingine, barabara ya Mheshimiwa Chenge wakati akichangia jana alizungumza juu ya barabara ambayo itakuwa ikitoka Lalago kuja Sibiti na pale Sibiti tutakuwa na route mbili, moja itapita Eyasi kwenda Karatu, lakini nyingine itapita Mkalama itakwenda Haydom - Katesh - Mbulu Mjini itakwenda hadi Karatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii ni barabara muhimu sana kwa sababu itaunganisha Mikoa kwa maana ya Simiyu, kwa maana ya Shinyanga, Mwanza, Singida na baadae tutakuwa na vipande vichache ambavyo vitaunganisha ukitoka Singida Mjini kwenda Mkalama, lakini ukitoka Singida Mjini kwenda Haydom. Kwa hiyo, unaona kwamba muunganiko wa barabara nchi nzima unakwenda vizuri na wale ndugu zangu wa Kigoma, maeneo ambayo yalikuwa yamebakia yako kwenye hatua nzuri kwa maana tutaiunganisha barabara kutoka Nyakanazi kuja Kibondo, unakuja Kidahwe mpaka Kigoma Mjini pamoja na matawi yanayounganisha nchi za jirani kwa maana sasa tunakwenda vizuri. Kwa hiyo, karibu maeneo mengi yanaunganishwa na hii ni itakuwa inatupa fursa kwenda kuunganisha barabara hizi ambazo tunaziita barabara za Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa maana hizi barabara za Wilaya ni barabara ambazo zinaunganisha Tarafa, makao Makuu ya tarafa na tarafa zingine, inaunganisha pia makao makuu ya kata na tarafa, inaunganisha pia kutoka kwenye kata na kwenda vijijini lakini pia na barabara za mitaa. Kwa maana hiyo sasa utaona kazi ambayo inafanyika na TARURA sasa hivi ni kufanya tathmini ya hali halisi ya ukubwa na mtandao wa barabara zetu kote nchini na hili zoezi linafanyika vizuri, liko hatua za mwisho sasa wanaendelea kuhakiki, zitakuwa na roughly na takribani kilometa 108,000. Sasa baada ya kukamilisha hiyo itatuwezesha sasa katika kupanga rasilimali hii kwa ajili ya uboreshaji wa barabara ili sasa tuje kuwa na mgao mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwahakikishie Wabunge na Bunge lako tukufu kazi kubwa inafanyika, ujio wa TARURA ni mkombozi kuhakikisha sasa uwiano wa barabara za kwetu unapata fedha vizuri na tunaendelea pia kuunganisha maeneo yaliyobakia ya nchi yetu pamoja na nchi za jirani. Ukiona hivi karibuni kuna mkataba umesainiwa pia ukitoka kule Mbinga kwenda Mbamba Bay, mkandarasi yuko site, lakini tunaunganisha na wenzetu upande wa Msumbiji naona Mheshimiwa Chief Whip wa kwetu hapa anazungumza, tutatoka Likuifusi tutakwenda Mkenda na tukitoka Mkenda tutarudi Tingi ili tuunganishe na barabara kubwa inayotoka kule Mbamba Bay lakini kule Mbamba Bay tutaunga na nchi za jirani pamoja na wenzetu wa Mbeya kwa maana ya ujenzi wa meli, lakini pia barabara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka pale Kitai ukienda Ruhuhu ziko kilometta 139 mwambao wa Ziwa Nyasa tunakwenda kuziboresha ili wananchi wa Ludewa waweze kwenda Kyela na kwenda Mbeya kwa wenzetu kule kwa maana muunganiko nilitaka nitoe mfano kwa maeneo machache muone namna Serikali inafanya juhudi ya kuunganisha Mikoa, lakini pia kutekeleza sera ambayo inataka tuanze kuunga Mikoa, tuunge na wenzetu wa nchi za nje ili tuweze kufungua fursa kwa sababu barabara pia itachangia katika maendeleo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme tu kwamba kitabu hiki cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri kimezungumza mambo mengi na niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge tusome. Barabara zimeanishwa vizuri, saa nyingine ninataka niseme hivyo kwa sababu yako maeneo ambayo tumetaja kwa mfano, uboreshaji wa miundombinu katika Jiji la Dar es salaam na upande wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kwamba wananchi wanahitaji wachangie katika uchumi wasikae muda mwingi barabarani ndiyo maana utaona nilikuwa nimejaribu kuonesha hapa maana yake nilishangaa juzi wakati Mheshimiwa Kubenea akichangia alisoma jedwali ila hakusoma kama Mheshimiwa Tambwe alizungumza hapa, alisoma jedwali akasema kuna barabara hewa nikaanza kushangaa nikitambua kwamba Mheshimiwa Kubenea ni mwandishi na nafikiri anahitaji kuwa makini zaidi ili saa nyingine ukizungumza jambo ulizungumze ukiwa na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukianda ukurasa wa 20 kama Mheshimiwa Tambwe alivyozungumza, Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake amesema wazi barabara ile ya Nzega - Puge - Tabora imetengewa fedha kwa ajili ya kumlipa mkandarasi, lakini yeye alisema kuna barabara hewa ambayo imekamilika na imetengewa fedha sasa hiyo siyo sahihi nilitaka niweke kumbukumbu sawa. Ni kwamba barabara zimeainishwa vizuri na mipango imeapangwa vizuri kwahiyo nilikuwa napenda Waheshimiwa Wabunge tukipitia tutaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nitoe mfano kwa upande huu wa barabara za Dar es Salaam, mtandao wa barabara ambao utakwenda kupunguza msongamano utakuwa na urefu wa kilometa 156 lakini ziko barabara ukitoka Tegeta tutakuwa tunakuja Mbezi sasa tunaendelea na usanifu, kutakuwa na barabara ambazo zitakuwa na njia sita. Lakini pia ukitoka Mbezi mwisho kwenda Pugu tunaendelea kufanya usanifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilitaka tu niseme kwa ufupi kwa sababu ya muda yako maelezo mazuri sana ukienda ukurasa wa 17 hadi ukurasa wa 21 tutaona namna tulivyojipanga ili kufanya mtandao wa barabara katika Jiji la Dar es salaam lakini pia upande wa Dodoma tumelitazama. Upande wa Dodoma tumejipanga kwa sababu ya uzoefu wa conjection katika Jiji la Dar es Salaam tumejipanga vizuri. Ziko barabara ambazo zimetajwa katika kitabu hiki utaona kuna barabara za mzunguko zina kilometa 104; lakini ziko pia barabara za ndani ambazo tutaziboresha ili Waheshimiwa Wabunge na wananchi wa Dodoma kwa ujumla waweze kupita na kufika katika maeneo yao na kuchangia katika uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona nitazama kwa sababu ya muda, sasa naomba nimalizie tu kwa kushukuru kwa nafasi hii lakini niwaombe Wabunge tu hata baada ya kikao tuweze kubadilishana mawazo hii nchi ni ya kwetu wote, kama kuna mawazo sisi kama Serikali tunayachukua kwa ajili ya kuyaboresha, muda wote tuzungumze, tubadilishane mawazo ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja hii ya asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mungu kwa nafasi hii, lakini nawapongeza Wizara ya Maji. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Mbarawa, nampongeza Naibu wake kwa kazi nzuri wanayofanya, pia nawapongeza watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu, Profesa Kitila Mkumbo kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Kwa kweli, maji ni uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu sisi katika Wizara ya Ujenzi tunapokuwa na miradi ya ujenzi wa barabara, tunahitaji kutumia maji kwa wingi. Kwanza sisi wenyewe kama sehemu ya kukamilisha miradi tunatumia maji, tunahitaji maji ya kutosha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapojenga barabara, madaraja makubwa, madaraja madogo, ma-calavat; pia tunapotengeneza madaraja haya ili kuweza kupitisha maji, maana iko mito midogo, mikubwa na iko mito ya msimu na ambayo inapitisha maji muda wote, tunahitaji maji katika kazi ya ujenzi kwa wingi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ili kushindilia barabara zetu zikae vizuri, maji yanatumika; ili kuweka zege katika maeneo mbalimbali, maji yanatumika; ili kuhakikisha kwamba barabara inakuwa stable, tunafanya curing kwa maana kwamba tunamwagilia maji na maji yanatumika kwa wingi sana. Kwa hiyo, upatikanaji wa maji huwa ni kigezo cha kupunguza au ku-control gharama za ujenzi wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukifanya shughuli za ujenzi wa barabara huwa tunawaelekeza makandarasi waweze kutengeneza au kujenga mabwawa ya kuhifadhi maji ili kukidhi mahitaji ya shughuli za ujenzi. Kazi hii ikikamilika, mabwawa haya hubaki na maeneo mengi tunatumia mabwawa haya yaliyobaki baada ya shughuli za ujenzi kwa shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi. Kwa hiyo, muda wote tunahitaji ku-manage maji ili tuweze pia kupunguza shida kubwa ya maji ambayo tunayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo ambayo pia tunachimba vifusi, tunachimba udongo ili kuweza kukamilisha shughuli za ujenzi wa barabara na baada ya ujenzi kukamilika na sisi kama Wizara hutoa mchango mkubwa wa kuhakikisha kwamba maeneo haya, hizi ball pits tunazifanyia marekebisho makubwa, tunazichonga vizuri ili ziweze kutumika kwa maeneo ambayo mahitaji ya maji ni makubwa sana. Kwa hiyo, huu utaratibu tunaufanya ili na sisi kutoa mchango katika kuhakikisha kwamba maji haya na hizi pits zinazobakia zinaweza kutumika kwa ajili ya kutoa huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme mbele ya Bunge lako hili kwamba uko uwezekano mkubwa wa kwamba sisi kama Wizara pale tunapotambua kuna mahitaji ya maji kwa wingi kiasi gani katika maeneo miradi ya barabara inapita tunazingatia kuanzia kwenye hatua ile ya usanifu tunaweka provision ili nasi tuweze kutoa mchango kwenye maeneo ambayo miradi ya barabara inapita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla kwamba sehemu ambayo tutakuwa na miradi kuanzia kwenye hatua ya usanifu watoe ushirikiano, watupe taarifa, lakini ninajua pia wako wadau wengine katika maeneo yetu, wakurugenzi na wananchi wenyewe wakitupa taarifa ili na hii fursa tuweze kuitumia na sisi kuendelea kupunguza adha ya maji ambayo yanahitajika kwa ajili ya shughuli za kibinadamu mbalimbali, shughuli za kilimo na pia kwa ajili ya kunyweshea wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko mifano ya miradi ambayo kwa ufupi tu niitaje. Baada ya miradi ya barabara kukamilika tumeacha huduma za maji kwa ajili ya kumbukumbu. Ukiangalia barabara ya kutoka Tabora – Puge kwenda Nzega yako maeneo mengi ambayo tumeacha mabwawa na sehemu nyingine tumeweka huduma ya maji. Barabara hii kutoka Nzega – Tinde kwenda Shinyanga kadhalika tunayo mabwawa ambayo yamebakia kandokando ya barabara, tunaendelea kuhudumia maji; barabara hii kutoka Nzega – Igunga – Shelui na penyewe yako maeneo ambayo tumeweka huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa maeneo pia ambayo yanazunguka kwenye Mji huu wa Dodoma kwa Barabara ya Dodoma – Manyoni – Singida, yako maeneo ambayo yanahudumia wakazi wa Dodoma na wakazi wengine wa Singida, tumeacha mabwawa ya maji. Ukiangalia pia, hata barabara kuu kutoka hapa Dodoma kwenda Morogoro, Dodoma – Kondoa – Babati, Dodoma – Iringa yako maeneo ambayo tumeweka huduma za maji. Kwa hiyo, nilitaka niseme tu kwamba fursa zipo kila wakati tupate hizi taarifa kuhusu mahitaji sahihi ya watu na sisi tutaendelea kutoa msaada wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunachimba visima kama sehemu ya social responsibility. Uko mfano, ukienda Kaliua kule kuna visima vitano tumechimba. Pia viko visima vingi kwa sababu, miradi ya barabara ni mingi, yako maeneo mbalimbali ambayo kama sehemu ya social responsibility tunatoa huduma kupitia wakandarasi wanaofanya shughuli hizi ili kuweza kutoa mchango mkubwa kwenye huduma za maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja zilitolewa hapa kwamba maji yanapotea katika maeneo mbalimbali. Hii ni kweli, tunapokuwa tumetengeneza ma-calavat na madaraja madogo, madaraja makubwa na pia kwenye hizi ball pit kuna maji yanapotea, kwa sababu, hatujajipanga vizuri kuhakikisha kwamba tunayatumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kutumia maji haya, siyo kazi ya Serikali peke yake, ni kazi yetu sisi wote. Wote tunao wajibu wa kushirikiana kuhakikisha kwamba tunayazuia maji haya yanayopotea kwa kiasi kikubwa kuliko maji yapotee halafu wananchi wana shida ya maji. Tukishirikiana kwa pamoja tutawahudumia vizuri wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwasihi na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge na kwa sababu pia, ziko mamlaka, TANROADS inajenga barabara, TARURA tunajenga barabara, lakini pia iko fursa ambayo tumepewa kupitia Bodi zetu za Barabara katika mikoa ambapo Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe; Wakuu wa Wilaya ni Wajumbe; wako pia Wenyeviti wa Halmashauri zetu za Manispaa na Majiji nao ni Wajumbe kwenye bodi hizi za barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba Waheshimiwa Wabunge tunapokuwa tunashiriki kwenye vikao hivi, basi mahitaji yetu, mipango yetu tuiweke kwenye bodi hizi ili nasi tuwe na sehemu nzuri ya kuchukua mahitaji haya. Kwa sababu kama nilivyosema, fursa ya kuendelea kutengeneza mabwawa haya yawe makubwa kulingana na mahitaji, nasi kama Wizara, uwezekano wa kutoa huduma hii ya maji upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tushirikiane ili sasa tukishatambua mahitaji yetu, kuliko kuyaacha maji yapotee, tunaweza sasa tukayatumia haya maji ili kuweza kuwahudumua wananchi sehemu mbalimbali. Kwa sababu tukiacha maji yakaenda, kwanza yanapotea bure, lakini tusipoya-manage pia yanaharibu makazi ya watu, yanaharibu mashamba na hata barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiona kama kuna vitu ambavyo vinahitaji na sisi tuvijue tuweze kuyatumia vizuri haya maji, nawaomba wote tushirikiane na wananchi, Waheshimiwa Wabunge na viongozi mbalimbali kwenye maeneo yetu tuweze kupata taarifa hizi ili sasa maji haya yaweze kutusaidia kuendesha shughuli mbalimbali za kibinadamu, yatumike kwa ajili ya mifugo na shughuli nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa na hayo kwa ufupi. Naomba sana katika hatua zote, kuanzia hatua za usanifu, pale tunaposanifu barabara huwa tuna-involve watu walio kwenye maeneo yetu. Kwa hiyo, hata tukiona kuna mradi wa usanifu unaendelea na kama tuna mahitaji ya maji, ni hapo naomba sasa tushirikiane ili mtuletee sasa mahitaji haya kwa pamoja tuyaingize kuanzia kwenye hatua za mwanzo ili saa hizi facility za mabwawa na sehemu ambazo maji yanapita na sisi mchango wetu uwe mkubwa kuhakikisha kwamba tatizo hili kubwa ambalo Mheshimiwa Profesa Mbarawa hapa anapambana nalo kupunguza shida ya maji, nasi kama Wizara ya Ujenzi tuko tayari kushirikiana na Wizara ya Maji ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuko tayari kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge ili maeneo yetu ambayo yana-demand kubwa ya maji na sisi kama Wizara ya Ujenzi tuendelee kutoa mchango wetu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja iliyo mbele yetu asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii muhimu. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu kwa asilimia mia moja. Pia nimshukuru sana Mwenyenzi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa leo. Nimshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa utashi na dhamira yake ya kweli ya kuwajali wanyonge hususan kwa kutengeneza miundombinu bora. Hii miundo mbinu itachangia kukuza uchumi na kupunguza umaskini kwa sababu huduma itakwenda kwa wafanyabiasha, wakulima, huduma za kijamii wafanyakazi na kadhalika.

Mheshimiwa Spika nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu kwa namna anavyosimamia shughuli za Bunge, lakini niruhusu nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi Mhandisi Isack Kamwelwe, kwa ushirikiano na miongozo anayonipa ili kutimiza majukumu yangu. Aidha, namshukuru pacha wangu Mheshimiwa Nditiye kwa namna tunavyoshirikiana katika kufanya kazi. Vile vile niwashukuru watendaji, Katibu Mkuu Arch. Elias Mwakalinga na Makatibu Wakuu wengine wote Leonard Chamuriho, Dkt. Maria Sasabo, Naibu Katibu Mawasiliano, Jim Yonaz na watendaji wengine wa Wizara nawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe mwenyewe, Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wenyeviti namna mnavyotupa ushirikiano katika kutekeleza majukumu yetu ya Wizara hii ya ujenzi. Pia inaishukuru Kamati yetu ya Miundombinu na Wabunge wote kwa ushirikiano wanaotupa ndani ya Bunge na hata nje ya Bunge. Tunaendelea kupokea maoni na ushauri wa Wabunge na sisi pia inatuboreshea kufanya kazi zetu. Vile vile niwashukuru wapiga kura wa Ushetu. Leo Madiwani wa Ushetu wapo hapa ni mashahidi, Madiwani wote hawa wa Chama cha Mapinduzi tunashirikiana vizuri na mimi kwa u-busy wangu Madiwani hawa kazi nyingi wanazifanya, Ushetu inakimbia kwa speed kubwa. Mwisho, niishukuru familia yangu Dkt. Macelina yupo hapa mke wangu, namshukuru sana kwa ushirikiano anaonipa katika shughuli zangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja zilikuwa nyingi lakini ni uhakika kwamba sio rahisi kuzungumza mambo mengi sana hapa, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge ushauri wao tumeupokea na yote waliyozungumza tutayajibu na kuyawasilisha kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, nizungumze mambo machache; kwanza kwa upande wa barabara; niseme tu kazi kubwa imefanyika, mtandao wa barabara nchi nzima barabara kuu za Kitaifa tuna kilometa 36,258. Kati ya hizo barabara kuu ni kilometa 12,176, barabara za mkoa ni kilometa 24,082, lakini kati ya barabara hizo kilometa 10,061 zipo sasa kwenye matandao wa lami kwa maana barabara kuu kilometa 8,870 na barabara za mkoa ni kilometa 1,756. Niseme tu kwa miradi inayoendelea hadi Aprili ni miradi 34 ambayo itakuwa na urefu wa kilometa 1,505 na hii miradi yote ikikamika ina- commit fedha nyingi kama Wabunge walivyosema trilioni 7.799, ni fedha nyingi, lakini katika bajeti hii tuliyowasilisha kutakuwa na ongezeko, tutakuwa na miradi kama 37 kwa maana tutakwenda kuhudumia barabara kwa ujenzi wa lami kilometa 1,961 na madaraja sita, hii ni achievement kubwa. Nitumie nafasi hii pia kumshukuru Mheshimiwa Rais zaidi na kumshukuru Waziri wa Fedha kwa sababu waanaendelea kutuwezesha na kazi kubwa inaendelea kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumze juu ya ujenzi wa viwanja vya ndege kwa ufupi. Waheshimiwa Wabunge wengi walivyokuwa wakichangia wamezungumza juu ya miradi ya fidia, lakini niseme kwamba, mwaka 2018 tulifanya uhuishaji wa uthamini ambao awali ulikuwa umefanyika mwaka 2007. Kwa hiyo, niwahakikishie tu Watanzania kwa ujumla kwamba kwenye maeneo ambayo kwamba tuna compensation kwa mujibu wa sharia, tunahuisha ili kuona tunakwenda kulipa compensation na wananchi wanapata haki yao.

Mheshimiwa Spika, kwa wachangiaji tulikuwa na Uwanja pia huu wa Ndege wa Msalato ambapo wapo waathirika ambao wanapisha ujenzi wa uwanja 1,926. Niwahakikishie kwamba takribani bilioni 14 ambazo tunazifanyia kazi ili waweze kulipwa hawa na kwa vile uelekeo wa kupata fedha ili kujenga uwanja huu upo, kwa hiyo wananchi hawa wa Dodoma husasan eneo la Msalato nao tumejipanga pia pamoja na wengine wa maeneo mengine watapata fidia zao.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo mengi ambao uthamini wa mali umeendelea; Lake Manyara, kule Simiyu, kule uwanja wa ndege wa Nyerere, Musoma na Songea. Katika maeneo haya yote Waheshimiwa Wabunge walichangia, lakini tumejipanga vizuri kuendelea kufanya malipo ya fidia, kwa sababu yapo maeneo mengi pia ambapo malipo yameshafanyika, kwa hiyo, tunaendelea kufanya uhakiki tukipata fedha tuanendea kulipa.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Waheshimiwa Wabunge pia wameuliza kwamba ni lini Serikali itaweka taa za kuongozea ndege. Kwa ufupi niseme kuwa, maeneo yote ambayo tunafanya maboresho ya viwanja vya ndege tutazingatia hili suala la kuweka taa za kuongozea ndege. Kwa hiyo katika maeneo mbalimbali ambayo tuna mradi kwa mfano kule Mafia na kule Songwe, taratibu za manunuzi zinakamilika mwezi wa tarehe 30 Aprili kwa hiyo tunaendelea kuharakisha ili tuende kufanya maboresho lakini katika maboresho tutazingatia mahitaji na vipaumbele ili viwanja hivi viweze kuwa bora na bora zaidi.

Mheshimiwa Spika, nizungumze pia kwamba uwanja wetu wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere unatarajia kukamilika mwishoni mwa mwezi huu wa Mei, 2019 na miradi ya ujenzi wa viwanja vya ndege vingine katika maeneo mengine tuko kwenye harakati ya kufanya maboresho; Uwanja wa Ndege wa Songea, Uwanja wa Ndege wa Mtwara, ujenzi unaendelea kule Geita, Mwanza Nachingwea na kama nilivyosema pia na upande wa Uwanja wa Songwe tufanya maboresho makubwa ya jengo la abiria. Naona Mheshimiwa Mwakajoka ananiangalia hapa, kwa hiyo tunakwenda vizuri katika uwanja huu ili tuweze kuufanyia maboresho makubwa.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge pia wameuliza kuhusu suala la ujenzi na ukarabati wa Viwanja vya Ndege vya Haydom, Kilwa Masoko, Lindi, Mafia, Manyara, Musoma, Mwanza na Tanga. Serikali inaendelea kutafuta fedha na pia inafanya mazungumzo na washirika mbalimbali wa maendeleo ikiwa ni pamoja na Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China na kadhalika kwa ajili ya ujenzi na ukarabari wa viwanja vyote vya ndege hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, nizungumze kidogo juu ya vivuko; ujenzi wa vivuko vipya viwili katika mwaka 2018/2019 umekamilika kwa maana ya Kivuko cha Kigongo- Busisi, MV Mwanza imekamilika na Magogoni - Kigamboni MV Kazi na pia tunaendelea kujenga vivuko vingine, kwa mfano ukarabati wa vivuko vitatu MV Sengerema, MV Kigamboni, MV Utete, lakini pia tunajenga kivuko kipya kitakachofanya huduma kati ya Kayenze na Benzi. Tumepanga vivuko hivi viweze pia ku-move kwenda pande nyingine, kivuko hiki kikikamilika ni cha kisasa, kitaweza kwenda maeneo ya Ukara kule Nansio kitatoa huduma katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, miradi mingine ya ujenzi wa maegesho ya Bwina kule Mkoani Geita maegesho ya kivuko kati Lindi na Kitunda, Mkoani Lindi, upanuzi wa maegesho Kigamboni pamoja na upanuzi wa jengo la kupumzika abiria. Kule ng’ambo Kigamboni tunaendelea kufanya maboresho, kuna mchangiaji mmoja hapa Mheshimiwa Mbunge alizungumza kwamba hakuna kinachoendelea, lakini tunaendelea kufanya maboresho, nafikiri labda hakuwepo muda mrefu, anaweza akajionea yeye mwenye kwamba tumejipanga vizuri ili huduma hii iweze kuboreka.

Mheshimiwa Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Tizeba amezungumza juu ya Kivuko cha Kome – Nyakalilo, tutafanya itakavyokuwa imewezekana kwa sababu tuna harakati za kujenga vivuko vingi, tunaona namna nzuri ili wananchi wapate huduma ya vivuko kulingana na mahitaji. Kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Tizeba kwa sababu tulipata ajali ya kivuko wakati tulikuwa tumelenga tumpelekee kivuko kwa sababu ya matatizo yaliyotokea, hivyo avumilie kidogo, tutaona namna nzuri ya ku-reallocate ili tuweze kupata huduma nzuri katika eneo hili la Kome kwenda Nyakalilo.

Mheshimiwa Spika, nizungumze juu ya maboresho makubwa na taasisi yetu ya TEMESA, Wabunge wengi wamezungumza, tunaendelea kuboresha, kumekuwa na changamoto na huduma za TEMESA, nakubaliana nao, lakini kama Wizara tumejipanga kuboresha karakana hii kwa maana ya kuongeza vitendea kazi na kuweka vifaa stahiki. Hata hivyo, kuna baadhi ya maeneo kwenye Wilaya kama kule Ifakara tumepeleka huduma na maeneo mengine tunaendelea kuwasogezea huduma wananchi ambao wanapata huduma hizi hususan taasisi za Serikali ili waweze kuzipata kwa ukaribu zaidi. Tunalenga kwenda kupeleka huduma hii katika Wilaya 25.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie juu ya huduma ya majengo na nyumba za Serikali. Imetolewa hoja kwamba gharama ni kubwa katika ujenzi, lakini nilikuwa nimejaribu kufanya mapitio kwamba pamoja na changamoto nyingi ambazo zipo kwenye TBA, Wizara inaendelea kushughulikia ikiwepo tatizo la wafanyakazi, tunaendelea kuongeza wafanyakazi ili tuweze kuboresha huduma hizi. Tulifanya utafiti kuona kwamba zile huduma za ujenzi bado zipo chini kwa miradi kadhaa, mfano, ujenzi wa mabweni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam tulijenga kwa bilioni 10, lakini wengine waliwasilisha gharama za ujenzi kwa bilioni 90. Pia gharama za ujenzi wa shule ya sekondari Ihungo wengine walituletea kwa bilioni 60 hadi 200, lakini Wakala walijenga kwa bilioni 12. Ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Geita bilioni 17 ndio TBA wanajenga, lakini wengine walituwekea bilioni 67. Sasa utaona gharama zipo chini kati ya wastani wa 30% hadi 40%.

Mheshimiwa Spika, niseme jambo moja hapa ambalo Waheshimiwa Wabunge walizungumza juu ya kufanya uchunguzi kuhusu baadhi mikataba ambayo imehusika kwenye ujenzi wa shule kongwe, sisi Wizara tupo tayari tutaunda timu ambayo itahusisha wafanyakazi wa AQRB, CRB na ERB ili kupitia upya mikataba yote na tuweze kupata ushauri kupata ushauri ili tuweze kuchukua hatua stahiki.

Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kusema Mheshimiwa Kingu alizungumza kwa uchungu hapa kuhusu barabara za Singida. Kwanza Mheshimiwa Kingu nimpe faraja kwamba katika bajeti hii tutatengezea barabara za mzunguko kwenye Mkoa Singida, kilometa 46 kwa mapendekezo ambayo yapo mbele ya meza. Hata hivyo, nimhakishie kwamba kwenye eneo la kutoka Singida kwenda Mgungila kwamba katika bajeti ya mwaka huu inayoendelea 2018/2019, tulikuwa tumetenga zaidi ya milioni 150 kwa ajili ya kuboresha, kujenga madaraja katika maeneo ambayo ni korofi na kuweza kuanza kunyanyua tuta. Kiasi cha fedha ambacho kinaonekana hapa ni kwa ajili ya kuendelea kufanya maboresho katika eneo hili na maeneo mengine, muda hautoshi, nafahamu kwamba yapo maeneo mengi ambayo kwenye Mkoa wa Singida kama alivyosema Mheshimiwa Kingu tunaendelea kufanya maboresho mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ningezungumza kidogo kwa kumalizia kuhusu ule mgawanyo wa fedha wa Mfuko wa Barabara. Niseme tu kwamba mgawanyo wa fedha upo kisheria, ni suala la kuangalia sheria lakini kwa upande wa Wizara kupitia, Bodi Mfuko wa Barabara tumeweka mshauri ili aweze kufanya mapitio tuone namna nzuri wa kufanya mgao huu wa fedha za TARURA na upande wa TANROADS. Hili zoezi linafanyika kwa sababu pale awali mgawo ulikuwa 80% kwa 20% kabla haujaenda 70% kwa 30% kwa mujibu wa sheria ilivyokuwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaendelea kukamilishia hili zoezi ili tuone urefu wa barabara, network nzima ili tuweze kuona matumizi ya barabara kwa sababu ndio bases kwamba ni vyombo vingapi, uzito upi unapita kwenye barabara zetu ili sasa tuweze kuona namna nzuri namna nzuri ya kufanya mgawanyo wa barabara hizi, pia tutazingatia hali ya jiografia. Ili twende vizuri wenzetu Wizara ya Fedha pia wanalifanyia kazi jambo hili na tukiweza kuongea fedha za ujenzi wa barabara tutaendelea kuziboresha barabara zetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana kwa nafasi hii na nimalizie kwa kusema kwamba, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba uniruhusu nimshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu na kuweza kuhitimisha hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru wewe mwenyewe kwa kutupa nafasi hii, lakini nakushukuru sana kwa kuweza kuongoza mjadala huu kwa umahiri na weledi mkubwa, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kurudia kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniteua, kuniamini na kunipa nafasi hii ili niweze kulitumikia Taifa kwa kuiongoza Wizara hii, namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nilikuwa na pacha wangu hapa, Mheshimiwa Mwanaidi, utaona kwamba nilikaa kwa utulivu. Unajua ukikaa na mama mambo yanakuwa barabara, sikuwa na pressure, nilikuwa napata ushauri wa kutosha. Kipekee nimshukuru sana, lakini pia nimefanya zoezi la kudumisha Muungano wetu. Ninamshukuru sana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata wachangiaji wengi, Waheshimiwa Wabunge 26 kama sikosei wamechangia kwa kuzungumza, nilipata pia michango ya Waheshimiwa Wabunge wawili ambao waliitoa kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda nitumie nafasi hii kuwapa pongezi nyingi sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao, lakini nipokee pia pongezi nyingi ambazo Waheshimiwa Wabunge mmezitoa kwa wingi sana, lakini pia mmewapongeza wenzangu hapa, Jenerali pamoja na timu yake na Wizara kwa ujumla. Kwa hiyo, hizo pongezi nazichukua na ninazifikisha kwa kweli kwa uzito ule ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, niwashukuru mmeonesha dhamira ya dhati ya kuona kwamba Wizara yangu inapata fedha za kutosha na sina mashaka Waheshimiwa Wabunge kwamba mtatupitishia bajeti hii ili twende tukafanye kazi yetu, tukatimize jukumu letu. Kikubwa hapa ni kuwashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu maneno yenu yametutia moyo sana, pia mmetupatia maeneo ambayo sisi tukitoka hapa kwa michango na ushauri wenu tunakwenda kuufanyia kazi, ninawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumshukuru sana Mheshimiwa Pinda, amezungumza kwa kirefu juu ya masuala ya ardhi. Lakini ninafikiri nianze na hilo na niongezee kidogo kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge, nimewasikia Waheshimiwa Wabunge, Mbunge wa Biharamulo umezungumza hapa juu ya eneo la Biharamulo na changamoto zake, na siyo hapa tu, Waheshimiwa Wabunge hawa tumekuwa na mijadala na majadiliano kule nje ya Bunge ili kuhakikisha kwamba changamoto ambazo zipo kwenye masuala ya ardhi tunakwenda kuzitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba nimewasikia, nimemsikia Mheshimiwa Mbunge wa Mtwara, nimekusikia ndugu yangu Mheshimiwa Tabasam kule Sengerema na ulizungumza na kunipa historia ya muda mrefu sana na maeneo mengi kwa kweli yenye mgogoro ni migogoro ambayo ilikuwa imekaa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi siiti mgogoro, naona tu kwamba ni changamoto ambazo zilijitokeza kwa sababu maeneo ya Jeshi ni mengi, tunayo maeneo mengi na wakati mwingine wananchi ulifika wakati wakaona labda saa nyingine hatuyahitaji, lakini maeneo yote tuliyokuwa nayo tunayo kwa ajili ya kuona kwamba lile jukumu la ulinzi linakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimewasikia Waheshimiwa kule Kyerwa na Katavi kwa Mheshimiwa Taska Mbogo, mchango wa maandishi wa Mheshimiwa Martha Mariki naye alizungumza kuhusu mgogoro ambao upo. Lakini kimsingi ninataka niseme tu kwamba katika maeneo yote tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo hili pia tulisikia kuhusu kule Kaboya kama sikosei, lakini pia tulikuwa tumezungumza hapa na ananitazama hapa Mheshimiwa Dkt. Bashiru kwamba ile issue ya maeneo yale, nitakwenda lakini taarifa ambazo zipo ni kwamba pia wenzetu wa milki, kwa sababu tulianzisha Kitengo cha Milki ili kurahisisha uratibu na kuhakikisha kwamba changamoto ambazo ziko kwenye maeneo ya ardhi tunakwenda kuzimaliza kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kuishukuru Serikali, tumepokea fedha kwa ajili ya kuifanya ile timu yetu ambayo inakwenda kuhakiki maeneo yetu ambayo yana changamoto, inakwenda kufanya kazi. Na nikuhakikishie tu kwamba kati ya maeneo 94 yaliyokuwa na changamoto likiwepo eneo ambalo Mheshimiwa Esther Matiko amelizungumza, lenyewe limefikia katika hatma yake, fedha zipo, wataalam wamekwenda, tunakwenda kulimaliza kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na maeneo yako mengine kama 44 hivi ambayo kwa sasa timu yetu ya milki imepata fedha kutoka Serikalini kwa ajili ya kwenda kumaliza mgogoro katika maeneo haya. Kwa hiyo, niseme maeneo yote Waheshimiwa Wabunge nimewasikia yaliyokuwa na changamoto ya migogoro hii ya ardhi, tutakwenda kuimaliza kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba nimepokea pia ombi la kwenda kwenye maeneo kadhaa, na baada ya Bunge lako hili tutakwenda kule na mimi napenda nikienda katika maeneo haya niende wataalam wakiwa wamemaliza changamoto zilizokuwepo kwenda kuwatia moyo wananchi wetu na kuhakikisha kwamba tunasonga mbele. Na tunafanya zoezi la kuhakikisha kwamba tumekwenda kutengeneza maeneo haya yawe na hati miliki. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Pinda kwa ufafanuzi wake kama alivyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie kidogo maeneo ambayo Kamati yetu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama imetoa mapendekezo hapa. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ni sikivu, na mimi ninaamini kabisa Waheshimiwa Wabunge Kamati hii ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama watakubaliana na mimi kwamba tumekuwa na mijadala mizuri ya kuhakikisha kwamba tunafanya Jeshi letu linakwenda kutekeleza majukumu yake kisawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote ambayo wameonesha kwenye ripoti, yako mengi ambayo tayari tumeshachukulia hatua nzuri, yako kwenye hatua nzuri na yako mengine ambayo yako kwenye mipango mizuri ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kuyatekeleza. Ninaamini kabisa maelekezo na ushauri wa Kamati utakwenda kutuboreshea utendaji kazi wetu katika Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kueleza machache yaliyoko kwenye ripoti ya Kamati, ninaomba nitoe ufafanuzi kwamba takwimu za utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2020/2021 ambazo nimezionesha zilikuwa ni kwa kipindi ambacho kinaishia hadi Aprili, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ninataka niseme kwamba kiwango kikubwa cha bajeti ambacho tumepokea baada ya Aprili, 2021 kwamba tumepokea fedha nyingi kwa ajili ya kukamilisha na kuendelea na shughuli zetu za mafunzo ya Jeshi, upande wa mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa, ukarabati wa miundombinu na shughuli za mashirika ambayo tunayasimamia katika Wizara. Kwa hiyo, tumeendelea kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Mambo ya Nje imeshauri pia Serikali ione umuhimu wa kutoa fedha za maendeleo kwa Fungu 39 kwa mtiririko uliopangwa, aidha, itoe kwa ukamilifu fedha zote za maendeleo ambazo bado hazijatolewa katika Fungu 38 – Ngome na Fungu 57 – Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niseme tu kwamba katika mwaka wa fedha 2020/2021, Fungu 39 liliidhinishiwa shilingi bilioni nne kwa fedha za maendeleo, lakini mpaka ninapozungumza tumepokea shilingi bilioni 3.5 na ushehe hivi. Kwa hiyo utaona kwamba karibu asilimia 100 ya fedha zote tulizotengewa tunazipata. Ninao uhakika mpaka tutakapokwenda kumaliza mwaka tutakuwa tumepokea asilimia 100. Naishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Fungu 57 – Wizara kupitia Fungu 58 – Ngome tumepokea shilingi bilioni 83.8 kati ya shilingi hizo bilioni 150. Lakini pia tulipokea shilingi bilioni 9.694 kati ya shilingi bilioni kumi mtawalia. Ninataka nioneshe tu kwamba kuanzia kipindi kile cha Aprili mpaka sasa hivi mtiririko wa fedha kwa kweli tunashukuru sana, ni mzuri. Tunakwenda vizuri sana.

Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tu kwamba ninaamini kabisa kwa makubaliano na Wizara ya Fedha kwa mazungumzo tulifanya na tukakubaliana, mpaka kufikia Juni tutakuwa tumefanya mapokezi makubwa na saa nyingine itakuwa kwenye rekodi nzuri katika kipindi hiki kwamba ninaweza nikasema haijawahi kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati pia ilitushauri kukamilisha mpango wa kuwapatia wahitimu wote wa kidato cha sita mafunzo ya JKT. Tunashukuru kwamba tumeendelea kupata fedha, ndiyo maana utaona kwa rekodi ya wanafunzi waliomaliza kidato cha sita kwa sasa hivi kwa fedha tulizopata tutakwenda kupokea wanafunzi hawa 35,000 ukilinganisha na kipindi kilichopita tulipokea wanafunzi 21,000. Kwa hiyo, unaona kwamba mambo yanakwenda barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipokea pia pesa kama nilivyosema, kwa ajili ya JKT, hizo shilingi bilioni 3.5 kati ya bilioni nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ilishauri kwamba tukamilishe haraka mpango wa kuwezesha vijana kujitolea kwa ajili ya mafunzo ya JKT kwa kuwapatia mitaji kwa kushirikiana na sekta na taasisi nyingine. Huo mpango ndiyo upo kama nilivyowahi kueleza hapo awali pia, kwamba tunafungamanisha sasa mafunzo haya ili tuweze kuwapokea watoto kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali zikiwemo Wizara kama ya Kilimo, Mifugo, Viwanda na Fedha ili tuone kwamba tutakuja na mpango kwamba vijana wetu wote ambao wanamaliza na kupata ujuzi tunakwenda kuwawezesha ili sasa yale mafunzo yao yalete maana kwa maana ya kwamba waweze kupata kazi ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niaombe tu Waheshimiwa Wabunge wakiwemo Wabunge vijana ambao mmezungumza kwa uchungu sana kuhakikisha kwamba hawa vijana ambao tunawaanda ili tutakapowarudisha wakirudi kule wakiwa wamepata mafunzo wamesheheni mambo mbalimbali, sasa waweze kwenda kujitegemea lakini pia kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi yetu. Kwa hiyo, mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala ambalo pia Kamati imetushauri kwamba katika miradi yetu Kamati imeona kwamba wakati mwingine tunapata fedha hizi za ufadhili zinakuwa na utaratibu wa kuwa labda imehitaji mshauri elekezi akatoka sehemu nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri huu pia tumeuchukua kwamba tutaendelea kuona kwamba tunaisimamia vizuri ili pale tunapopata fedha au tumefadhiliwa, lakini mshauri mwelekezi awe sehemu yetu ili tuweze kufanya kulingana na mahitaji yetu. Kwa hiyo na hilo tumeweza kulichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, upo mchango Waheshimiwa Wabunge wamezungumza juu ya kuliimarisha Shirika letu la Nyumbu pamoja na mashirika mengine. Nataka niseme tu kwamba tunayo mashirika, tuna Shirika letu hilo la Nyumbu (TATC), lakini pia tuna Shirika letu la Mzinga na SUMA JKT.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumza juu ya Shirika letu hili la Nyumbu, kwanza tumepata fedha ambapo sisi wenyewe kupitia Nyumbu tunakwenda kutengeneza nguzo zile za umeme na kazi imeanza. Naishukuru sana Serikali, tumepata fedha za kutosha kwa ajili ya kufanya maboresho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mpango wa kwenda kufanya ufufuaji, ip0 mitambo 116 ambayo kipindi cha nyuma ilifanya kazi vizuri, lakini pia kwa kuzingatia mabadiliko ya teknolojia; upande wa Serikali tumejipanga vizuri, tumepata ule mpango wa maendeleo kwa ajili ya kuinyanyua Nyumbu. Na hii imekubalika Serikalini sasa tunakwenda kufanya maboresho makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, yako mambo mengi yatakwenda kufanyika kule Nyumbu na tunapenda pia Nyumbu iwe kitovu. Tutakwenda pia kuzingatia kuwachukua vijana ambao watakuwa na weledi wa tofauti, wabunifu. Tutajitahidi kuhakikisha kwamba tunaifanya iwe center wale vijana wote ambao tunaona wanaweza kuwa na uwezo wa kitofauti tutawachukua. Lakini kazi yetu sisi ni kuwatengeneza na pia kuweza kuwatoa katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuona kwamba ule ujuzi wao tunauendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejipanga vizuri, tunakwenda kuiboresha Nyumbu na tutakwenda kuweka fedha za kutosha kabisa na utaratibu unakwenda sawasawa. Kwa hiyo Nyumbu tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Mzinga tunafanya uzalishaji – Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanachangia, Mheshimiwa Ahmed alichanganya kidogo Nyumbu na Mzinga; Mzinga ndiyo tunazalisha yale mazao muhimu. (Makofi)

Kwa hiyo, tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tunakwenda kufanya sasa uzalishaji wa mazao ya kutosha kwa sababu sisi wenyewe mahitaji ya yale mazao ni makubwa sana, lakini bado ziko taasisi nyingi za kiulinzi hapa nchini zinahitaji kupata huduma ya kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali pia muda siyo mrefu tumepokea fedha nyingi sana na tumeshaagiza mitambo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kuzalisha kwa hali ya juu, kwa hiyo tumejipanga vizuri. Kule Mzinga tutakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mengine ambayo tunakwenda kufanya maboresho kama nilivyozungumza, kule SUMA JKT. Kwa sababu taasisi zetu hizi zimejipanga sasa kwenda kufanya uzalishaji wa hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo niwatoe hofu tu kwamba tumejipanga kweli kweli na yako maeneo mengine tutakwenda kufanya maboresho ya sheria zetu ili kufanya taasisi zetu zifanye kazi, zitumie weledi, tuwatumie wataalam tuliokuwa nao vizuri bila kuwa na kikwazo chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo haya yote yanalenga kuhakikisha kwamba ile historia ambayo Waheshimiwa Wabunge mmekuwa mkiirejea kwamba tunayo historia ya taasisi zetu hizi kipindi cha nyuma tuliweza kutengeneza magari, tuliweza kutengeneza mpaka nyambizi, tutakwenda kufanya hivyo. Lakini tutakwenda kujikita zaidi pia kwenye eneo hili la utafiti, na ndiyo maana upande wa Serikali tumejiandaa na tulikuwa na andiko ambalo niko nalo hapa ambalo linalenga kwenda kuboresha taasisi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla niseme kwamba Wabunge walivyochangia nilikuwa najaribu kuangalia, angalau kuweka kwenye ma-group maeneo ambayo wamezungumza, kwa ujumla wake nikijaribu kupitia ninaona kwamba kulikuwa na masuala ya bajeti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumza. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, lakini niseme tu kwa hali ya bajeti hii ambayo naiombea sasa hivi hapa kumekuwa na ongezeko la bilioni 217 kama nilivyozungumza, hii ni asilimia kumi, siyo haba. Lakini bado Serikali imeonesha nia kwamba huko tunakokwenda tutakwenda kufanya maboresho makubwa sana ya ongezeko la bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sana kwa concerns zenu, lakini naishukuru pia Kamati kwa sababu Kamati imezungumza vizuri sana na kutoa maelekezo. Kwa sababu uko umuhimu wa kupata fedha za kutosha ili hizi zana ambazo tunazimiliki tuweze kuzitunza, tuweze kuzifanyia mazoezi, kwa sababu ili tuweze kuwa vizuri zaidi upande wa mazoezi ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa masuala ya kibajeti mmezungumza masuala ya pensheni. Tumeanza kughughulikia suala la pensheni, tumeanza na level ya Major Generals na Lieutenant General na majenerali kuhakikisha kwamba ile sheria ambayo ilipitishwa tunakwenda kuitekeleza. Kwa hiyo, tunaendelea kuifanyia kazi kuona maslahi ya askari wetu tunayaweka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia yale masuala ya pensheni Waheshimiwa Wabunge mmezungumza hapa tunachukua ushauri wenu, lakini pia mmetoa pia masuala ya kibajeti juu ya ununuzi wa vifaa na hili tupo nalo vizuri, vifaa vya kwetu tulivyokuwanavyo tunavyo vya kisasa, tupo vizuri. Waheshimiwa Wabunge msiwe na wasiwasi, tupo vizuri. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge wamezungumza pia juu ya stahili za wanajeshi ni kweli zipo changamoto, lakini upo ukweli kwamba changamoto hizi tumezizungumza wenzetu wa Hazina, na ni ukweli kwamba tumewasilisha mahitaji yetu na mahitaji ya wanajeshi wetu ambayo wanadai na uhakiki unaendelea kukamilishwa kwa sababu tayari tumeshakuwa na mwelekeo na makubaliano kwamba tutakwenda kulipa haya madeni ya vijana wetu ambayo yamekaa muda mrefu. (Makofi)

Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge nimewasikia na imetia moyo kuona mnawajali sana vijana wetu, Jeshi hili ni la kwetu, vijana hawa ni wa kwetu, lazima tuwahudumie ili waweze kutufanyika kazi nzuri, waendelee kufanya kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuhusu stahili zao na maboresho ya maslahi niliambie tu Bunge lako na mimi mwenyewe nipo mstari wa mbele kuhakikisha kwamba ninakuwa na jeshi ambalo ni la kisasa lakini jeshi ambalo linahudumiwa na jeshi ambalo sasa linakuwa na morali na motisha ya kutosha kwenda kufanya kazi. (Makofi)

Kwa hiyo, hili halina wasiwasi tumefanya vikao kadhaa kwa nia ya kufanya maboresho. Waheshimiwa Wabunge, niwatoe hofu tunakwenda kufanya mapinduzi makubwa ili jeshi letu hili zuri lenye sifa nzuri tuendelee kuona kwamba tunawatendea haki vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kuhusu maeneo mengine ambayo Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla mmechangia ni juu ya mafunzo ya JKT, Mheshimiwa Musukuma ulizungumza sifa, sifa zipo ndiyo maana tunaonesha sifa ya vijana wa kujitolea tumeionesha kuanzia darasa la saba tunakwenda, kwa sababu tunakata hata yule kijana ambaye hakubahatika kwenda shule, lakini akija kwetu tutamtengeneza, akirudi kule kijijini anakwenda kufanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sifa zipo zinamuonyesha kijana ambaye tutaweza kumchukua kwa ajili ya kujitolea na wale vijana kwa mujibu wa sheria. Kama mlivyozungumza kwamba sifa zipo tutaendelea kufanya hivyo, pale ambao patalazimika kuwa na kutengeneza sifa za ziada kulingana na mazingira ambayo tupo nayo tutafanya hivyo kwa nia hiyo hiyo yakuona kwamba tunaendelea kuwatengenezea vijana sifa nzuri, uzalendo, uchapakazi na kuweza kutoa mchango wao kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nimuarifu tu Mheshimiwa Matiko hapa alizungumza kwamba kuna deni kule SUMA guard, labda hii rekodi ya miaka mingi lakini mpaka ninapozungumza sasa hivi kwa vijana ambao wameajiriwa huko SUMA guard hatuna deni. Kwa hiyo hii, kama labda saa nyingine sikukuelewa naomba tu baadaye tunaweza tukazungumza nikupate sawa sawa, eeh si ndiyo haina mashaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme tu pia ipo michango ilitolewa kuhusu ushirikiano wa JKT na JKU na ushauri uliotoka Mheshimiwa tumeupokea lakini niseme tu, nakuliarifu Bunge lako tangu mwaka 2001 yapo mashirikiano ambayo tunayafanya, tunabadilishana uzoefu, tunabadilishana mafunzo, tunabadilishana hata vijana kwa ajili ya kuona kwamba tunakwenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwatoe wasiwasi ndugu zangu na mimi hata nimetembelea kule Zanzibar na nina programu za kwenda Zanzibar pia, kwa hiyo nikitembelea kule nitaendelea pia kufanya mijadala kwa ni hiyo hiyo ya kuona kwamba tunafanya majeshi yetu yanafanya kazi kwa ushirikiano wa hali ya juu ili kuona kwamba sisi wote tunakwenda sawa, kwa hiyo, Unguja nilikwenda na Pemba nitakwenda siyo mara moja, nitaendelea kwenda kwa nia hiyo hiyo ya kuona kwamba tunaweza kujiweka vizuri ili tuone kwamba tunatembea wote pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ongezeko la bajeti kama nilivyozungumza kwa ajili ya mafunzo kule JKT na pia kuna ushauri uliotolewa kwa ajili ya elimu ya muungano kupitia majeshi yetu tutaendelea kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nilikuwa naona record pia ya bajeti hata ya JKT kwa maana ya mafunzo kwa mujibu wa sheria imeongezeka kutoka shilingi bilioni 16 kwenda bilioni 21.6 hii siyo jambo dogo, nilijaribu kuonyesha tu kwamba tunajitahidi sana kuomba fedha ili tuendane sambamba na mahitaji ya kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mambo mengine ambayo yalizungumzwa kwa ujumla ilikuwa ni ujenzi na ukarabati wa miundombinu ushauri tumeuuchukua, hata mimi nimetembelea hizi nyumba katika maeneo kadhaa tunahitaji kupaka rangi, tunahitaji kufanya maboresho na hiyo ni jambo la kawaida. Huwezi kujenga nyumba ukakaa nayo muda wote bila kuwa uliifanyia ukarabati na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mapungufu kadhaa ambayo tumeyaona hata tulivyokuwa na Kamati, tumejipanga kwenda kushughulikia upungufu wa nyumba lakini upo mpango pia wa kuendelea kujenga nyumba kwa ajili ya wanajeshi wetu, mmeshuhudia nyumba nyingi zimejengwa kwa kipindi kifupi, lakini mpango ule siyo kwamba umeisha tunaendelea kwenda kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengine walizungumza juu ya mchango wa jeshi letu kwa ajili ya ulinzi wa amani. lakini pia Mheshimiwa Lucy Mayenga alizungumza juu ya kuongeza idadi ya akinamama katika operation zetu. Niwahahakishie tu asilimia 6.5 ya wanajeshi waliopo kwenye operation tunao akinamama, yapo mahitaji mengine ni maalum yanahitaji akinamama wanajeshi kuwasaidia wenzetu katika maeneo ya operation. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kunapokuwa na machafuko maeneo kadhaa waathirika wakubwa ni akina mama na watoto, tunahitaji pia kuwa na weledi kupitia jeshi letu kuweza kusaidia. Kwa hiyo tutaendelea kuongeza idadi kadri itakavyokuwa kwa sababu yapo makubaliano ambayo tunayafanya na wenzetu tunapokuwa tunapeleka askari kwenye operation. Kwa hiyo, tutaendelea kuona hivyo na tunafanya mijadala mingi ili kuona kwamba tunakidhi mahitaji ya wanajeshi wetu katika ulinzi wa amani katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, kama nilivyozungumza juu ya upimaji na uthamini wa ardhi kwamba mambo tumechukua lakini Wabunge wengi pia walizungumza juu ya huduma za afya, ndiyo maana tumejipanga na Waheshimiwa Wabunge msiwe na wasiwasi kwa wale ambao mngeweza kupata nafasi ya kutembelea kule Lugalo mnaweza kuona kwamba tumetengeneza eneo maalum kwa ajili ya kumudu magonjwa hatari ikiwemo Ebola na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kule utaona, tunavyo vifaa maalum. Mheshimiwa Kuchauka, yapo maeneo ukifika kule utashangaa maana yake mimi nilishangaa na mimi kidogo nina uzoefu kidogo, sasa wewe uliyetoka Liwale nafikiri ukienda kule nikukaribishe uone mambo mazuri ambayo yanafanyika kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejipanga kwa ajili ya kupokea hatari yoyote ikitokea kwa sababu wanajeshi wetu wanapokwenda kwenye operation pia kuna maeneo yana hatari sana, kwa hiyo tumejipanga hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi ya hapo kama nilivyozungumza kwenye hotuba yangu asilimia 80 ya huduma tunazotoa kwenye hospitali zetu ni kwa raia wetu kwa watanzania wenzetu. Kwa hiyo, unaona kwamba tunavyoimarisha hospitali zetu inalengo pia ya kwenda kuwahudumia wananchi wa watanzania na tunaendelea kufanya hivyo ndiyo maana tumeona kwa sababu Serikali sasa imehamia hapa Dodoma tumeanza ujenzi pale Msalato na ujenzi huu fedha tunazo, tutasimamia kuhakikisha hospitali hii inakamilika ili sasa tuweze kugawana kutoa huduma katika maeneo ya kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sidhani muda upo kwenye nafasi yangu, nimalizie tu, kukushukuru sana, nikushukuru sana kwa kuendesha mjadala, lakini Waheshimiwa Wabunge nimeona leo wametulia sana, kwa hiyo, ninawashukuru sana, walikuwa makini sana na nilifikiria kwamba saa nyingine tutakuwa na wachangiaji wachache, lakini tumepata michango mingi sana, na saa nyingine niseme tu siyo rahisi michango yote niweze kuizungumza moja kwa moja, lakini niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge tumewasikia na leo timu yangu ilikuwa kubwa kwa sababu ya kuhakikisha kwamba hatuachi neno hata la Mheshimiwa Mbunge mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ndiyo jeshi letu, jeshi letu limejipanga vizuri kama mnavyoliona hakuna mashaka, jambo lolote Waheshimiwa Wabunge mmelizungumza hapa tunaenda kulifanyia kazi kwetu sisi ndiyo mmetupa kazi ya kuweza kuhakikisha kwamba tunawatumikia watanzania kwa weledi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kuwapongeza sana Katibu Mkuu yupo hapa na viongozi wote wa Jeshi wapo hapa, kazi nzuri inafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepata nafasi kadhaa ya kuzungumza na wenzetu kutoka nje ya nchi na kwenye mashirika mbalimbali, jeshi letu linatamanisha sana liwepo maeneo mengi, mchango wake ni mkubwa na mchango wake ni mzuri sana, jeshi letu lipo katika ubora wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa NaibU Spika, kwa hiyo mimi naendelea kuwapongeza najisikia furaha sana kuwa Waziri katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa kutoa hoja.

WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa kunipa nafasi ili
niweze kuchangia kwenye taarifa za Kamati ya Nishati na Madini na ile ya Miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii nipongeze sana kamati zote hizi mbili
kwa kuja na ripoti nzuri; ripoti ambazo ukizisoma zimesheheni mapendekezo mazuri sana na
maazimio mazuri kwenye ripoti hizi na imani yangu kwamba Serikali itafanyia kazi na
kuyatekeleza vema mapendekezo ambayo yapo kwenye ripoti ya Kamati hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya ya miundombinu pamoja na nishati na madini
ni muhimu sana katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Stadi zinaonesha asilimia 80
ya uwezeshaji wa uwekezaji inatokana na nishati hizi pamoja na miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkazo mkubwa ukiwekwa kwenye sekta hizi
utachochea kiasi kikubwa sana cha maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimboni kwangu Ushetu hatuna umeme, tumebahatika kuwa
na vijiji vitatu tu ambavyo vimepata umeme, imekuwa ni vigumu sana kushawishi wawekezaji
kuja kuweka uwekezaji wa aina mbalimbali. Kwa hiyo, ninaamini kabisa katika hii REA III kwa vile
vijiji vyangu vimeonekana kwenye ule mpango basi nafikiri Mheshimiwa Waziri hapa
atanihakikishia kwamba tutapata umeme ili ile kasi ya kuvutia wawekezaji katika maeneo ya
kwetu tuweze na sisi kuweza kusukuma katika maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ninasema ni muhimu katika ukuaji wa uchumi; hivi
majuzi tulikuwa tunazungumza juu parameter mbalimbali za ukuaji wa uchumi ikiwemo
mfumuko wa bei; nilitaka nijikite hapa kidogo nizungumze na namna ambavyo hata wakati
mwingine bei hii ya nishati ya umeme na mafuta inavyoweza kuathiri; kuna muda wa kutafsiri hili
suala la mfumuko wa bei.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu utakuja kuona mfumuko wa bei umekuwa
mkubwa sana katika hizi nishati za petroli, mafuta ya taa pamoja na vitu vinavyoambatana na
petroli. Kwa mfano kwa ripoti za BOT zinaonyesha kwamba kwa mwezi ule wa Oktoba na
Novemba mfumuko wa bei umepanda sana kwenye nishati hii ya mafuta na umeme kutoka
asilimia 6.2 kwenye asilimia 11.7. Sasa utakuja kuona kwamba hii ndio maana wakati mwingine inaleteleza tukitafsiri mfumuko wa bei inakuwa haieleweki kwa watumiaji hasa kule vijijini kwa
sababu utaona kwamba maeneo mengine kumekuwa na mfumuko katika rate ndogo, lakini hii
ukija kuchanganya kwa ujumla wake utakuja kuona unapata wastani wa nne nukta tano
mpaka nne nukta nane katika mwezi ule tu wa kutoka mwezi wa kumi kwenda mwezi wa kumi
na moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukizungumza juu ya hali ilivyo vijijini saa nyingine inaweza
isieleweke sasa nataka niseme kwamba upo umuhimu sasa wa Serikali kutazama eneo hili la
nishati ili kuweza kuudhibiti huu mfumuko katika maeneo haya ya nishati ili ule uwiano wa ujumla
ulete maana halisi. Kwa hiyo, nilikuwa naona hii ni sehemu muhimu sana kwamba Serikali iweze
kuiangalia. Kwa sababu ukiona upandaji wa gharama hizi za nishati za mafuta na umeme
zinasababisha ukuaji ambao uko shaghala bagala katika maeneo mbalimbali ya utumiaji kama
kwenye chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nilikuwa najaribu kuangalia ripoti hii utaona
kabisa kwamba wakati mfumuko wa bei unapanda kwenye nishati hii, bei ya chakula inakuwa
ni shida. Nilikuwa najaribu kuona katika kipindi kirefu kwa mfano, nimeangalia kipindi cha mwezi
Mei mpaka Oktoba, 2016 hii ilikuwa imeshuka inflation katika eneo hili. Lakini kipindi kilichofuata
baada ya Oktoba kume-shoot sana katika nishati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali naishauri ijaribu kuangalia kwa sababu nishati
hii inavyopanda, bei ya chakula inapanda ukizingatia kwamba wananchi wetu sasa
kwasababu ya miundombinu iliyopo mjini sehemu ambayo kuna umeme kumekuwa na
uzalishaji wa vyakula na bidhaa nyingine zimekuwa bora zaidi. Kwa hiyo, wananchi wanauza
mazao yao yanakuja mjini halafu baadae yanarudi kwa ajili ya utumiaji kule; kwa hiyo
kunakuwa kuna athari kubwa ndio maana tunaona kwamba bei ya chakula inakuwa ni shida.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nizungumze eneo lingine kwa sababu natoka maeneo
ya uzalishaji wa chakula, umuhimu wa matumizi ya nishati yetu katika kutengeneza mbolea,
niishauri tu Serikali kwamba ilitazame eneo hili ili uzalishaji wa mbolea uwe kwa wingi ndani ya
nchi lakini pia wananchi tuweze kupata mbolea kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka pia nijue kwamba ule mradi wa kutengeneza
mbolea ya Urea ambao kulikuwa kuna majadiliano kati ya TPDC na wale Wajerumani umefikia
wapi kwa sababu sisi ndiyo matumaini yetu. Katika msimu huu hatukupata kabisa mbolea,
tulipata mbolea kwa ajili ya kilimo cha tumbaku, wakulima wa mahindi hawajapata mbolea
sasa na wananchi wameitika vizuri sana kutumia hizi pembejeo. Na kwa kweli inatia matumaini
kwa sababu sasa wananchi wanaweza kuzalisha hadi gunia 30 kwa eka kama watawezeshwa.
Kwa hiyo, nilitaka niisemee Serikali itazame uzalishaji wa mbolea kwa kutumia hizi nishati zetu za
gesi asili ili mbolea ipatikane kwa wingi wananchi waweze kupata mbolea na kuweza kufanya
uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kusaidia wachimbaji wadogo, maeneo
ninayotoka tuna maeneo ambayo wachimbaji wadogo wanachimba. Sasa ni ombi langu tu
kwa Serikali kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni isaidie kuweka mazingira
mazuri kwa wachimbaji wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kwa kusema naunga mkono hoja hizi, Serikali iweze
kutusaidia tuweze kusonga mbele. Ahsante.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuunga mkono hoja. Napenda kutoa mchango wangu kwa kuishauri Wizara hii kusimamia fedha wanazochangia wananchi wakulima wa tumbaku kupitia tozo kwenye mauzo yao namna zinavyotumika kwenye kuhifadhi Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa wabunge wajue tozo ni kiasi gani zimekusanywa na kiasi hicho kimerejeshwa kwenye maeneo yaliyoathirika na uharibifu wa mazingira; kwani kuna uwezekano zikatengenezwa taarifa za fedha zilizotumika ambazo siyo sahihi kwani wananchi binafsi wanajihusisha kuhifadhi mazingira. Isije ikatokea kuwa na utaratibu hafifu fedha za tozo kwenye tumbaku zikatumika na wajanja na wakasingizia zimetumika kwa kubadilisha na juhudi binafsi za wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tumehamia Makao Makuu ya Halmashauri ya Ushetu, Makao Makuu katika Kijiji cha Nyamilangano (Jimbo la Ushetu) na kwa kuwa Mahakama inayohudumia eneo hili yako mbali na kwa kuwa tunayo Ofisi ya OCD – Ushetu tuliyopewa hivi karibuni na ni muhimu mashauri mbalimbali yanaelekezwa umbali mrefu kupata huduma za Kimahakama na kwa kuwa Halmashauri ya Ushetu iko tayari kutoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama tunaomba Serikali itujengee Mahakama ya Mwanzo eneo hili la Kijiji cha Nyamilangano (Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya Ushetu) ili wananchi wapate huduma ya haki zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja. Naomba kuchangia mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ahadi ya Rais, ujenzi wa barabara ya lami. Wakati wa kampeni Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliahidi ujenzi wa barabara ya lami kilometa 10 Ushetu. Je, barabara hii itajengwa lini ukizingatia Jimbo la Ushetu halina barabara hata mita moja? Zaidi kuna vumbi jingi sana Makao Makuu ya Halmashauri ya Ushetu. Naomba Serikali itilie mkazo ujenzi wa barabara kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ujenzi wa minara ya mawasiliano. Halmashauri yetu ni mpya, tumefanikiwa kuwa na Wilaya ya Kipolisi, tumehamia Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya, Kijiji cha Nyamilangano, Kata ya Nyamilangano. Mawasiliano ni hafifu na tunapata shida kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ya TEHAMA yanakwama ikiwemo mfumo wa malipo na mifumo mingine ya Halmashauri ya Wilaya yetu. Inalazimika wakati mwingine kazi zifanyikie kwenye Halmashauri huko Mjini Kahama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ya kudhibiti usalama kwa Jeshi letu la Polisi pamoja na ulinzi shirikishi; niliwahi kuwa na swali nikaomba Kata za Nyamilangano, Uyogo, Chona, Ushetu na Kata nyingine, Serikali itusaidie tupate minara ili tukimbizane na maendeleo katika Jimbo la Ushetu. Naomba sana priority iwe Makao Makuu, yaani Kijiji cha Nyamilangano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kupandisha hadhi barabara; tumekuwa na maombi ya kupandishiwa barabara hadi ya TANROAD barabara zinazounganisha mikoa hususani:-

(i) Barabara ya kutoka Tulelo - Mhulidede - Tabora kilometa 21. Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Shinyanga na Tabora.

(ii) Barabara ya Chambo hadi Mambari. Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Shinyanga hadi Tabora.

(iii) Barabara ya Masumbwe (Mbongwe – Geita), Mwabomba, Ulowa, Kaliua (Tabora). Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Geita, Shinyanga hadi Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi ni muhimu kwani maeneo haya yatachochea utalii, tutasafirisha mazao ya chakula na biashara na mambo mengi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, kuhuisha Kamusi ya Barabara; naomba sana Wizara hii ihuishe Kamusi ya Barabara kwani inatunyima fursa ya kugawanya rasilimali vizuri. Mfano, Kamusi inayotumika, inaonyesha Ushetu ina mtandao wa barabara wa kilometa 416 tu wakati hali halisi tuna mtandao wa barabara kilometa 1,600. Tunaomba Serikali iboreshe Kamusi ya Barabara ili tushughulikie barabara na kupewa rasilimali kwa mtawanyiko ulio mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba mambo hayo manne yashughulikiwe. Ahsante na naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Ushetu lina vituo vya tiba 27 na linahudumia wananchi zaidi ya 300,000 kulingana na sensa ya mwaka 2012 na lina ukubwa kilometa za mraba 5,311. Kati ya vituo hivyo vya tiba kuna vituo vya afya vitatu vya Mbika, Ukune na Bulungwa. Kati ya vituo hivyo vituo viwili vya Mbika-Ushetu na Bulungwa vina huduma ya upasuaji, vituo hivi vinahudumia watu wengi sana kwa kuwa watu wa Jimbo la Ushetu wanahudumiwa na Hospitali ya Wilaya ya Kahama ambayo imezidiwa sana kwani inahudumia Halmashauri nyingi ikiwemo Halmashauri za Ushetu, Ulyankulu, Kaliva, Uyui, Bukene, Mbogwe, Msalala na maeneo ya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo niiombe Serikali ifikirie kupandisha Kituo cha Afya cha Mbika-Ushetu kuwa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ili kusaidia mzigo mkubwa unaobebwa na Hospitali ya Wilaya ya Kahama. Hivyo kuanzishwa au kupandishwa hadhi kituo cha afya kutasaidia mambo mengi ikiwa ni pamoja na kupunguza vifo kutokana na wananchi kusafiri umbali mrefu kwenda Hospitali ya Wilaya kwa kata za Ushetu, Uyogo, Nyamilagano, Ulowa, Ubagwe pamoja na wananchi wa majimbo ya Kaliua, Ulyankulu, Uyui ambao hutibiwa Kahama Mjini kupitia maeneo ya Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itaondoa dhana kwa wananchi kuona kwamba wametengwa. Vilevile itaboresha huduma za afya Jimboni Ushetu pamoja na kupunguza mrundikano katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali itusaidie kupata ambulance ili kuokoa maisha ya wananchi wa Jimbo la Ushetu. Sisi kama Jimbo au Halmashauri tunajitahidi kujenga ili kupata zahanati nyingi katika harakati za kutekeleza sera ya kuwa na zahanati kila kijiji. Kwa sasa tunayo majengo 48 yanayoendelea kujengwa kwa nguvu za wananchi na Halmashauri yao. Majengo hayo ni zahanati 44 na nyumba za watumishi nne. Tunaomba tusaidiwe gari ya kubeba wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu gari ya chanjo, Halmashauri ya Ushetu haina gari ya chanjo, tunaiomba Serikali itusaidie gari ya chanjo katika Halmashauri ya Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mko hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kukuomba Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii na Mheshimiwa Naibu Waziri mtembelee wananchi wa pembezoni mwa Hifadhi ya Kigosi/Moyowosi yaani pembezoni mwa Halmashauri ya Ushetu - Kahama, Mkoani Shinyanga hususan Kata za Ulowa, Ubagwe, Ulewe, Nyankende na Idahuria, mjionee shida zilizopo; mikakati ya uhifadhi shirikishi, uonevu, mawazo mazuri ya wananchi, eneo lililopoteza sifa na upungufu wa eneo la malisho. Ziara itahamasisha sana uhifadhi maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Serikali iweke mipaka inayoonekana kwenye hifadhi zetu kama inavyotajwa na Section 28 ya Sheria Na. 14 ya Hifadhi ya Misitu ya mwaka 2002. Hii itasaidia kupunguza migogoro kwani wananchi wataona kirahisi na kuiheshimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Section 29 ya Sheria na 14 ya Hifadhi ya Misitu ya mwaka 2002 (Forest Act, 2002) inampa nafasi Mheshimiwa Waziri kupitia mara kwa mara hifadhi za misitu yetu na kuifuta ile ambayo imekosa sifa. Namuomba Mheshimiwa Waziri/Serikali ifanye mapitio ya eneo la Msitu wa Usumbwe (Usumbwe Forest) ililolitwaa mwaka 1966 na kuliunga na Hifadhi ya Kigosi/Moyowosi kwani msitu huu hauna sifa; urejeshwe ili wananchi watumie kuwa malisho, bwawa la kunyweshea na kilimo cha umwagiliaji. Hii itasaidia kutokuwa na uharibifu wa hifadhi yetu ya Kigosi/Moyowosi na kupandisha uchumi wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Chuo cha VETA Ushetu, nchi yetu imekuja na dhamira ya kuifanya Tanzania iwe nchi ya uchumi wa kati na nchi ya viwanda. Hii itafanya wananchi kupunguza hali ya umaskini. Pia kufanikiwa ajenda hii, jitihada zifanyike ila siyo tu kutoa ajira hususan kwa vijana bali ni kuhakikisha nguvu kazi inatumika kwenye uzalishaji. Hivyo kunahitaji vijana wetu wawe na skills za kutosha kutoa mchango wao muhimu kwa ukuaji wa uchumi. Hivyo tunaomba Serikali yetu itujengee Chuo cha VETA katika Halmashauri ya Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ushetu inazo fursa za kutosha kufanya chuo hicho kilete tija kwa kuwa eneo hili ni kiungo kwa vile tunapakana na mikoa mitatu ya Geita, Kigoma, Tabora pamoja na Shinyanga yenyewe. Ni rahisi wananchi wa mikoa hii kufika Ushetu.

Pili, Ushetu kunapatikana rasilimali za kutosha za mazao ya misitu, mazao ya kilimo na kadhalika.

Tatu, Ushetu kunapatikana ardhi ya kutosha ambayo haina gharama. Wananchi wake wanao ushirikiano na wanajituma na wanapenda sana maendeleo.

Mhehimiwa Spika, namalizia kwa kusema tunomba sana Chuo cha VETA haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja. Bidhaa zinazoingizwa bila kukidhi viwango.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kushauri kuwa vifaa vinavyokamatwa kutoka nchi za nje kama mabati ambayo tatizo lake ni Specfication, yaani geji isiyokuwa sahihi badala ya kuviharibu vitiwe chapa ya bei kulingana na hali yake halisi ili vitumike kwa shughuli nyingine kama kujengea mabanda ya mifugo kuwekea fensi pia ujenzi wa nyumba za muda mfupi. Kuviharibu ni kupunguza level ya uchumi na vina impact kwenye GDP kwani kuna fedha zimetumika toka kwa wazawa (domestic).

Mheshimiwa Naibu Spika, bei za bidhaa kuwa juu (bidhaa za viwanda vyetu). Wizara hii ishirikiane na Wizara ya Fedha kulinda bei ya bidhaa inayotengenezwa ndani; kuweka VAT kwenye bidhaa inayoanza kuzalishwa nchini na kupandisha bidhaa hiyo kwa walaji wa ndani kwa kuwa inamvutia mzalishaji kuuza nje ya nchi kwa ajili ya zero rated concept ya export zote. Pia kupoteza ushindani kwa bidhaa inayozalishwa au kuingizwa kutoka nje hususani nje kwenye upatikanaji wa material ya bei rahisi, technology ya hali ya juu na sera zao juu ya exports zao. Nashauri VAT itazamwe vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya pembejeo. Nashauri Wizara iweke mkazo sana kwenye viwanda vitakavyozalisha pembejeo, yaani mbolea, madawa pamoja na vifaa vya kilimo. Pia maduka ya vifaa vya kilimo yawekwe maeneo ya wakulima sambamba na mafunzo kwa wananchi ili wajue au wapate elimu ya umuhimu wa kutumia vifaa vya kisasa kuwawezesha kuwa na kilimo chenye Tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hii hoja muhimu ya maji. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitasema mawili tu kwa haraka haraka. Kwanza kikubwa ni kuishukuru Wizara kwa sababu Jimbo la Ushetu ni Jimbo ambalo liko katika Wilaya hii ya Kahama, lakini utaona kipindi kilipita tumekuwa na shida kubwa sana ya maji na kwenye bajeti hii ambayo tunaitekeleza niseme wananchi wa Ushetu wanashukuru kwamba tumekuwepo na miradi kwenye kata nane na katika kata tatu tayari wananchi wameanza kupata maji. Kwa hiyo, naishukuru sana na kuipongeza Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kata hizi za Idahina, Ukune, Chambo, Bulungwa, Nyamilangano, Kinamapula Kata ya Ushetu yenyewe na Kata ya Ulowa, tulitenga fedha mwaka 2016/2017, kwa hiyo, naiomba Serikali iendelee kukamilisha hii miradi ambayo inaendelea ili wananchi waendelee kunufaika na kuachana na adha ya ukosefu wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka nizungumzie, wananchi wa Ushetu wanahitaji maji ya Ziwa Victoria. Kama nilivyosema kipindi kilichopita, Jimbo la Ushetu linachukua eneo la asilimia 57 ya Wilaya ya Kahama, lakini maji ya mradi wa Ziwa Victoria yamefika Kahama Mjini, lakini maji haya hayajasambazwa Ushetu. Wananchi wa Ushetu wanaomba maji ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa sababu wataalam wa Wizara wako hapa, nikumbushe, kulikuwa kuna maombi ya maji mwaka 2014, tuliahidiwa kwamba Mkandarasi Mshauri angeenda kwa ajili ya kusanifu ili maji yaende Ushetu. Sasa mradi uliishia njiani. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iangalie ili tuweze kupata maji katika Kata za Ukune, Kisuke, Nyamilangano, Uyogo, Ushetu na Ulowa; na kuna vijiji vipatavyo 32. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri pia kwenye mradi wa maji ambao utakuwa ukipitia kwa majirani zetu katika Halmashauri ya Mbogwe, sehemu ya Masumbwe, tunaweza pia tukapeleka maji kwenye Kata za Idahina, Igwamanoni, Nyankende ambako kuna vijiji 40 vinaweza kunufaika. Kwa sababu lengo la Wizara au la Serikali ni kuhakikisha kwamba mwaka 2020 tunaweza kuwa na maji vijijini kwa asilimia 85. Kama hatupati maji ya Ziwa Victoria itakuwa ni ndoto. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali izingatie hili na nimefanya mazungumzo na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji namshukuru sana na naamini yale tuliyokubaliana kwa ajili ya kutusaidia Ushetu ataweza kutusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu nizungumze juu ya ubora wa report za miradi. Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wamekuwa wakizungumza wanaona kwamba miradi inajirudia, lakini utagundua kwamba ile reporting system yetu tuiangalie vizuri, Wizara ya Fedha isaidie kwamba twende kwenye IPSAS accrual ili tuweze kupata report ambazo zitakuwa zinaleta maana. Kwa maana ya mchanganyiko wa cash basis na accruals inatuchanganya sana. Kwa mfano utaona kwa upande wa Halmashauri ya Ushetu tumepokea fedha shilingi bilioni 506 lakini haiwezi kueleweka mapema kwamba hizi fedha zilikuwa zimetengwa mwaka upi wa fedha. Kwa hiyo tukienda vizuri kwenye hizi report itaweza ku-report miradi yetu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naishauri tu Wizara ya Fedha isaidie sana ili hizi report za miradi ziende kwenye ile reporting system ambayo nafikiri itakuwa ni nzuri zaidi ili kututoa katika mchanganyiko ambao tunaweza kukanganyikiwa zaidi. Kwa hiyo, nafikiria niseme hili, kwa sababu nimeona maeneo mengi sana yamekuwa yakituchanganya; tukienda kwenye accrual ziko faida nyingi. Hii itaweza pia kutusaidia kuoanisha bajeti na matumizi kwa kipindi husika. Kwa hali ilivyo sasa hivi mchanganyiko unakuwa ni mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda nishauri kwamba, tume-adopt accrual basis of accounting, kwa hiyo, nafikiri Serikali isukume sana ili zoezi likamilike, itatusaidia sana kuweza kupata report zenye ubora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri, nashukuru Serikali kwa kuendelea kutuboreshea huduma za maji katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji toka Ziwa Viktoria. Utakumbuka maji ya Ziwa Viktoria yamefika katika Mji wa Kahama na yanapelekwa Nzega na Tabora lakini hayakusambazwa Jimbo la Ushetu ambalo liko Wilayani Kahama. Jimbo la Ushetu linashikilia 57% ya eneo la Kahama, wananchi wa Ushetu wanahisi kutengwa kwani maji haya yanawazunguka. Pia maji yanayotoka Mto Malagarasi watayatazama tu majirani zao wa Halmashauri ya Ushetu. Kwa kuwa tulifanya kikao na Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalam wa Wizara tarehe 3/5/2017 na kugundua kuwa tulikuwa tumeahidiwa kuunganishwa mwaka 2014, naiomba Wizara ianze tena mchakato wa kutuletea maji katika Halmashauri ya Ushetu toka mradi wa Ziwa Viktoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, umwagiliaji. Naiomba Wizara iongeze juhudi za utafiti ili tuweze kutafiti maeneo ambayo tunaweza kutengeneza mabwawa ili yasaidie kwenye kilimo cha umwagiliaji. Ushetu tunayo maeneo yenye rutuba na ambayo yanafaa kuweka skimu za umwagiliaji. Maeneo hayo ni kwenye Kata za Uyogo, Idahina na Sabasabini. Wizara itusaidie utaalam huo na kuelekeza nguvu ili tuweze kuchangia malighafi za viwanda vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mipya. Utaratibu wa kutekeleza miradi mipya iliyotengewa fedha haujaeleweka kwani Halmashauri zinasubiri fedha ili kuweka kandarasi. Tunaomba zoezi lisimamiwe vema na sisi Wabunge tushirikishwe ili miradi ianze kwa wakati na certificate zitoke ili miradi ikamilishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kupata nafasi ya kuchangia hoja zilizo mbele yetu, lakini nitajikita kwenye eneo moja tu la miundombinu, hususan sekta ya ujenzi. Nimshukuru sana Mwenyekiti wa kamati na kamati nzima kwa kweli, kwa muda wote ushauri wao na maelekezo yao na kwa kiasi kikubwa tuliyazingatia na kwa kweli, yametupa ufanisi maeneo mengi. Na ndio maana Mheshimiwa Mwenyekiti hapa wakati wa kuwasilisha ametoa shukrani kuona Serikali inafanya kazi kubwa na kuweza kutekeleza pia, maoni ya kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipongeze tu Bunge kwa ujumla. Nasoma ripoti, nimezisoma ripoti tangu tulivyoanza kuzipokea katika Bunge lako, lakini utaona kuna maboresho makubwa sana. Na hata ukiiangalia ripoti ya wenzetu Kamati ya Miundombinu utaona kumekuwa na mabiresho makubwa. Hata maoni yake ambayo tumeyapokea ni maoni ambayo yanalenga kwenda kutuboreshea shughuli zetu, lakini pia ni maoni ambayo yanatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya ujenzi ni muhimu kwa sababu ni sekta wezeshi, inatoa huduma kwenye ukuaji wa viwanda, kwenye kilimo na kwenye huduma mbalimbali kwa hiyo, tumepokea maoni ya kamati. Na maeneo ambayo yalikuwa yameguswa ni upande wa TANROADS, upande wa barabara, ujenzi wa viwanja vya ndege, upande wa Wakala wa Majengo Tanzania, pia tumepokea maoni kwenye Chuo cha Ujenzi Morogoro na Chuo cha Mafunzo ya Teknolojia Stahiki Nguvu Kazi kule Mbeya, lakini pia upande wa wakala wa ufundi na umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufundi kabisa tumeona changamoto ambazo kamati imezitaja. Nilihakikishie Bunge lako ushauri huu mzuri sana tutaendelea kuuzingatia, ili tuone kwamba tunakwenda kufanya maboresho makubwa, lakini kwa lengo hilohilo la kuona kwamba, tunaendeleza mkakati wetu wa kuwa wezeshi, ili kuweza kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo kadhaa Waheshimiwa Wabunge pia, wakati wakichangia hoja hii wameyazungumza, lakini niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, changamoto za barabara, hususan kwenye kipindi hiki cha mvua nyingi na kamati imetushauri kwamba, tuangalie mtazamo kwamba, kipindi cha miaka hii ambapo mvua inakuwa nyingi pia, ile bajeti yetu upande wa dharura tunaweza kuiweka, lakini kimsingi ukiuangalia bajeti zetu tunavyoziunda tunakuwa tunapangilia hivyo kwamba, kuna maeneo korofi, kuna maeneo ujenzi wake ni wa muda. Tukitoa mwanya kwamba, wakati tukiwa tunazingatia kwamba, tumetenga fedha kwa ajili ya periodic maintenance kwa maana hiyohiyo kwamba, yako maeneo mengine ambayo kurejeshea miundombinu inategemea pia, kwamba, hali ya mvua iwe imepungua. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kwa maeneo ambayo tunaona bado tuna changamoto na mvua imekuwa nyingi kwamba, tutakwenda kufanya marejesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokuwa nikizungumza mara nyingi kwa utaratibu wa kibajeti kama Mheshimiwa Waziri wa Fedha alivyozungumza tunafanya mawasiliano. Kwa sababu, tulikuwa na bajeti ya bilioni 8.2 kwa ajili ya dharura, lakini hadi kufikia mwezi wa kwanza mwanzoni tulikuwa tuna mahitaji ya kwenda kwenye bilioni 15, lakini hivi ninavyozungumza kumekuwa na mvua nyingi zimenyesha kwenye Mikoa ya Mara kule, lakini mvua nyingi zimenyesha pia, kule Simiyu. Tunaendelea kupokea shida mbalimbali kwenye maeneo mengi, lakini niwahakikishie tu kwa sababu, Serikali inazingatia kuona watu wanapita katika maeneo yao kwenye changamoto za barabara niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumejipanga kuwasiliana na wenzetu upande wa Wizara ya Fedha kwa utaratibu wa kibajeti, ili tuende kurejeshea mahitaji ya sehemu ambazo zimeharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimalize tu kwa kusema kwamba, Waheshimiwa Wabunge michango yao yote waliyoisema sisi tumeichukua kwa nia hiyo ya kwenda kufanya maboresho. Na nimalizie kwa kusema naishukuru sana Kamati na tutaendelea muda wote kusikiliza maoni ya kamati kwa nia hiyohiyo ya kufanya maboresho makubwa na ninaunga mkono hoja ambazo ziko mbele yetu, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania wa Mwaka 2018
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kusema naunga hoja zote hizi mbili zilizo mbele yako. Namshukuru pia Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu pamoja na Wajumbe, pia Waheshimiwa Wabunge ambao walihudhuria kwenye vikao vya Kamati na kutuboreshea Muswada huu. Nitazungumza mambo mawili tu; la kwanza nataka nizungumze upande ule wa ukaguzi hasa kwenye Muswada huu wa usafiri wa barabarani kwa maana ya kwamba ukaguzi ambao utafanywa na Mamlaka hii ya LATRA na lile suala la ukaguzi kupitia vyombo vyetu vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Muswada huu ni kudhibiti usafishaji barabarani kwa maana LATRA wata shughulika na suala la controls kwa maana kudhibiti na suala la Polisi kukagua magari barabarani wenyewe wanaangalia utekelezaji wa sheria maana yake compliance ya sheria wakiwa barabarani. Kwa hiyo hapa hakuna mwingiliano, kama ilivyo kwenye taaluma zingine ukiwa Daktari ukisha- graduate kuna Bodi ambayo inakutazama kwenye utekelezaji wa majukumu yako kama Daktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu madereva wameonekana kama ni watu ambao hawathaminiwi. Kwa maana hii sasa tunaichukua kama ni taaluma ili waweze kudhibitiwa. Tunajua kuwa na leseni ni jambo lingine lakini kuitumia vizuri kitaaluma leseni yako ni jambo ambalo LATRA wataenda kulitazama, kwa maana mtu awe na leseni lakini lazima tumwone pia anafanya kazi zake na kutufanya tuwe salama pia tukiwa huko barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka nizungumzie kuhusu mizani, kwamba sisi kama Serikali tumejipanga kuendelea kuboresha mizani zetu katika sehemu mbalimbali kwa maana ya kuzifanya ziwe za kisasa na kuzifanya zifanye kazi kwa tija na kufanya watumiaji wa barabara wasitumie muda mwingi wa kuwa barabarani, kwa sababu vituo vitakuwa vichache. Juhudi mbalimbali zinaendelea na kuna maeneo ambayo nafikiri Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla tunaendelea kufanya maboresho makubwa kwenye mizani zetu. Waheshimiwa Wabunge watakubaliana na mimi kwamba uko umuhimu wa kuzilinda barabara zetu na uwepo wa mizani hizi ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti na kuhakikisha barabara zetu ambazo tunatumia fedha nyingi kuzitengeneza zinabakia kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto ambazo zimekuwepo muda mrefu kwenye matumizi ya mizani barabani, lakini niseme tu Serikali imekuwa ikifanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba tunafanya maboresho na kuondoa changamoto ambazo muda mrefu zilikuwa zinatukabili huko barabarani. Kwa hiyo, nikuhakikishie na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumedhamiria kufanya ubora mkubwa katika udhibiti wa barabara zetu kwa kutumia mizani za kisasa, halafu kutakuwa na tija, usumbufu utakuwa mchache na watumiaji wa barabara hawatatumia muda mwingi watakapokuwa wakitumia barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa sababu ya muda, nimalizie tena kwa kutoa shukrani kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja zote zilizoko mbele ya meza yako. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili name niweze kuchangia katika hotuba hii muhimu na ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nianze kwa kuunga mkono hoja hii asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na ninaomba uniruhusu pia nimfikishie salamu za Watanzania walio wengi, kila mahali tulipotembelea miradi, tumekuwa tukipokea pongezi na salamu za wananchi wakisema kufikishe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, pongezi kwa Mheshimiwa Rais. Nami nitumie nafasi hii niziwasilishe salamu na pongezi kutoka kwa wananchi, kwa sababu wanatambua kwamba Serikali yao ya Awamu ya Tano kwa kuimarisha miundombinu ya usafiri na usafirishaji ndiyo kiunganishi muhimu cha sekta za uchumi katika nchi hii na kwamba ni kichocheo katika kukua kwa uchumi na maendeleo ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nizungumze tu kama ufafanuzi kwa Waheshimiwa Wabunge. Kwanza nianze kwa kuwapongeza kwa michango mizuri na utashuhudia kwamba uchangiaji wa bajeti una mabadiliko makubwa sana. Kwa hiyo, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa sababu kwa sehemu kubwa tumepokea ushauri na sehemu kubwa tumepokea maelekezo ya Waheshimiwa Wabunge katika kutekeleza majukumu yetu, wanafanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo, nami nawapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla na yale yote ambayo wameyatoa kama ushauri, nasi kama Serikali na kama Wizara pia tutaendelea kuyatekeleza.

Mheshimiwa Spika, nifafanue tu mambo mawili ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi walizungumza hasa hoja ya kuimarisha miundombinu iliyoharibiwa na mvua katika kipindi hiki ambacho tumepokea mvua nyingi. Niseme tu kwamba Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu hasa ya barabara na madaraja yaliyoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha nchini kuanzia kipindi cha Oktoba, 2019 mpaka mwezi Machi.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba tumejipanga kwa maana ya kuendelea kurejeshea miundombinu. Ukiangalia kwa ujumla wake, ukubwa wake kwa kipindi hiki kulikuwa kuna makadirio kama ya shilingi bilioni 34.3 ambapo upande wa TARURA ilikuwa kama shilingi bilioni 40 na upande wa TANROAD shilingi bilioni 34. Kwa hiyo, utaona athari hizi zimetuchota mafungu makubwa sana kuendelea kuimarisha.

Mheshimiwa Spika, kubwa niseme tu kwamba tumejipanga vizuri kuhakikisha Serikali inaendelea kurejesha miundombinu ili ile sera ya kuhakikisha wananchi wanapita na kwenda kwenye shughuli zao za maendeleo, ziendelee bila kupata kikwazo chochote.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie barabara hii muhimu ambayo Mheshimiwa Lubeleje alikuwa ameizungumzia. Hii barabara utakubaliana nami kwamba ni barabara muhimu. Ni barabara inayotuunganisha kutoka Mbande kwenda Kongwa - Mpwapwa mpaka kule Kibakwe. Hii barabara tulishaifanyia usanifu kwa ajili ya kufanya matengenezo. Kwa sasa shughuli za ujenzi zinaendelea, Mkandarasi aliyeko kwenye site amekamilisha kilometa tano na zile kilometa nyingine 11.7 kukamilisha kilometa 16.5 kwenda mpaka Kongwa ikifika mwezi wa Tano natumaini kwamba tutakamilisha barabara hii.

Mheshimiwa Spika, vile vile uko ujenzi wa kilometa mbili ukitoka Mpwapwa kuja Kongwa unaendelea vizuri na tumeshasaini mkataba na Mkandarasi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Lubeleje na wananchi wa maeneo hayo tuliyoyataja wasiwe na wasiwasi, tumejipanga vizuri kuona kwamba tunaendelea kupeleka huduma hii muhimu ya barabara kuelekea Mpwapwa na siyo Mpwapwa peke yake, kwenda mpaka maeneo mengine ambayo tunajua yanayo uzalishaji mkubwa na huduma hii ni muhimu sana kwa Wananchi wa maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Lubeleje pia alizungumza juu ya madaraja muhimu sana haya; kule Godegode, Mpwapwa, Nyasungwi na Mbande. Niseme tu, katika mwaka wa fedha huu ambao tunaokwenda nao tulitenga fedha na kazi ya usanifu wa madaraja hayo ulishakamilika. Tunaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba tunarejesha madaraja haya muhimu ambayo Mheshimiwa Lubeleje ameyataja, nasi tunayaangalia kwa macho mawili.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwa ujumla wake, Dodoma ni kati ya Mikoa ambayo imeshambuliwa sana na hizi mvua nyingi tulizozipata. Kwa hiyo, utaona Dodoma ni kubwa, maeneo mengi yalikuwa yamepata athari za mvua. Niwahakikishie tu wakazi wa Dodoma na Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla kwamba tumejipanga kuhakikisha tunaenda kufanya maboresho makubwa kwenye maeneo haya ambayo yameharibiwa; siyo hapa Dodoma tu, lakini na maeneo mengine ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka nichangie hayo kwa sababu ya muda, lakini niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tutakwenda kufanya maboresho ya miundombinu hii. Yumkini katika bajeti inayokuja pia tutaonyesha namna tulivyojipanga ili maeneo yote haya yaliyopata athari za mvua tutakavyoyafanyia urejeshaji kupitia bajeti.

Mheshimiwa Spika, naamini Bunge lako litatupitishia fedha ili tuende kufanya kazi kubwa kuhakikisha wananchi wanarudishiwa huduma muhimu za miundombinu ya usafiri na usafirishaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, narudia tena kusema naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ni hotuba nzuri na bajeti nzuri ili tuende tukafanye kazi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kutoa shukrani zangu kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye hoja hii muhimu. Nianze kwa kuunga mkono hoja na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Biteko na timu yake na Wizara ya Madini kwa ujumla kwa ushirikiano ambao wanatoa kwa Wizara tunapotekeleza majukumu yetu. Kwa hiyo, nawapongeza na kuwashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba, tumepewa jukumu la kulinda mgodi wetu wa Tanzanite kule Mererani, lakini labda niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, pia ni kwa mujibu wa Ibara ya Katiba ya…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nimeshawaomba tena na tena; eeh, taratibu.

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, utanilinda dakika yangu.

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 105 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi inatupa fursa ya kuendeleza kusimamia ulinzi na maeneo ambayo ni muhimu ya kimkakati. Kwa mgodi huu tunaoulinda pia kwa maelekezo ya Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yetu ya Ulinzi na Usalama, tunalinda kule Mererani.

Mheshimiwa Spika, niseme, ukipewa kazi ya ulinzi, siyo jambo dogo na hasa lazima tuzingatie weledi ili tuweze kuvuka salama. Kwa hiyo, jeshi letu linafanya kazi nzuri, uniruhusu niwapongeze sana Askari walioko kwenye maeneo haya, wanafanya kazi kubwa kwa uadilifu wa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kuna changamoto nyingi, lakini vijana hawa ambao wako kwenye eneo la Mererani kwa ujumla, Mheshimiwa Mbunge alijaribu kukumbusha hapa kwamba tunakagua watu kati ya 8,000 na 10,000, lakini kwa hali halisi ukienda kwenye eneo tunakagua zaidi ya 10,000. Kuna siku ambazo tunakwenda mpaka kukagua watu 15,000 kwenda 20,000; na tulikuwa tuna sehemu mbili tu za kukagulia.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Wizara ya Madini kwamba baada ya kuwa na maombi ya kuongeza maeneo ya ukaguzi, sasa kuna vyumba takribani 10 vinaongezwa ili tuendelee kuboresha ulinzi katika eneo hili. Kwa hiyo, vijana walioko pale wanafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, ukifanya kazi ya ukaguzi unalazimika wakati mwingine kufanya upekuzi na hii ni kawaida pale ambapo unakuwa na mashaka. Mashaka yanatoa uthibitisho kwamba, saa nyingine tutakapokuwa na mashaka tunakamata haya madini ingawaje Waheshimiwa Wabunge hapa umesikia wakizungumza kwamba, labda ni kidogo kidogo; lakini hiyo kidogo tunayokamata kwangu mimi naamini kwamba inazuia madini kuvushwa kwa wingi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba tutaendelea kufanya kazi hiyo, lakini tunavyofanya ulinzi, tunafanya doria, lakini tukiwa katika maeneo ya ulinzi tunashirikisha vyombo hivi vya ulinzi mbalimbali. Kwa hiyo, hatuko peke yetu. Mheshimiwa Mbunge Ole-Sendeka hapa rafiki yangu amezungumza hapa na kwa uchungu mkubwa, lakini niseme tu kwamba kazi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ole-Sendeka atakumbuka kwamba tulivyotembelea tukiwa na Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Mheshimiwa Ole-Sendeka namshukuru, alikuja na tulikwenda kukagua sehemu ya ukaguzi tukiwa na Mheshimiwa Mbunge. Nawapongeza sana Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa sababu ya namna nzuri walivyofanya kumshirikisha Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Mbunge alitoa hoja zake na rai yake kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, pia tarehe 12 mwezi wa Nne wakati tulikwenda kwenye Kamati kujibu maelekezo ya kamati baada ya ziara ile ya tarehe 16 mwezi wa Tatu, tulikuwa tumepata maagizo ambayo ninayo; yako maagizo 13 ya Kamati; na kati ya maagizo yaliyokuwepo, liko agizo la kufunga scanner katika maeneo ya ukaguzi ambalo wenzetu wa Utumishi na Utawala Bora wanalifanyia kazi. Tutakapopata scanner tutakwenda kutoka kwenye hii tradition way ya kukagua, tuanze kukagua kisasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Ole-Sendeka alipata nafasi wakati wa ziara na wakati wa Kamati. Haya maelekezo yaliyotoka kwenye Kamati ninaamini kabisa Mheshimiwa Ole-Sendeka yana mchango wake kwenye Kamati. Nami naamini hivyo kwamba tunaendelea kuyafanyia kazi. Niseme kati ya maagizo haya, yako maagizo sita ambayo tayari tulishayatekeleza kwa kushirikiana na Wizara ya Madini, vile vile yako mengine ambayo yako kwenye hatua, tunaendelea kuyatekeleza.

Mheshimiwa Spika, naomba wananchi na wachimbaji waendelee kutoa ushirikiano kwa vyombo vyetu. Vyombo vyetu vinafanya kazi kwa weledi na kwa uzalendo wa hali ya juu na saa nyingine tutawasikitisha kuwaletea tuhuma au niseme kuwaletea maneno ambayo yatawakatisha tamaa.

Mheshimiwa Spika, mimi kama nimepewa dhamana kwenye Wizara hii, nitaendelea kusimamia maelekezo ya Kamati, nitaendelea pia kusikiliza Waheshimiwa Wabunge na nimhakikishie tu Mheshimiwa Ole-Sendeka kwamba tuko pamoja kwenye jambo hili, pale ambapo tutapata scanner tutakwenda kufanya ukaguzi kwa staha na kwa uzalendo na kwa kushirikiana na wananchi. Ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini wa Mwaka 2016
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye Muswada huu wa Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini wa mwaka 2016. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kutujalia afya, nimepata fursa hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Wizara, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalam kwa kuja na muswada huu. Kwa kweli huu muswada umekuja ukiwa umechelewa, ulitakiwa uje wakati ule tunaanza kufanya reforms mbalimbali, kwa sababu unakuja sasa kutuondolea matatizo mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada huu unajaribu kutoa kielelezo cha utawala bora kwa sababu tutakapokuwa na Sheria hii ya Uthamini kuna mambo mengi yatakuwa kwa uwazi na itaongeza pia uwajibikaji katika usimamiaji wa hizi rasilimali ikiwemo ardhi, nyumba na assets nyingine ambazo zimetajwa kwenye sheria hii. Pia inaongeza dhana nzima ile ya ushirikishaji, kwamba inatoa fursa ya kushirikisha makundi mbalimbali. Kwa hiyo, nilifikiria nianze kwa kuipongeza sana Serikali kuja na muswada huu na nina uhakika kuna mambo mengi yatakaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niseme tu faida chache kwa sababu yapo mambo mengi sana, kutokana na muda niseme tu faida chache ambazo ninaona zitaenda kuondolewa na kuwa na muswada huu. Kwanza utaona kabisa kwamba ili kuweza kutoa ile risk iliyokuwepo kwenye assets zetu kwamba wakati mwingine kulikuwa kuna over valuation wakati labda rasilimali au mali za Serikali zikinunuliwa na labda wakati mwingine kulikuwa na undervaluation wakati mali za Serikali zikiuzwa. Kwa hiyo, hii itaenda kutibu na utaona kabisa kwamba kwenye ile section ya 49 inaonesha kabisa kwamba kutakuwa na vigezo vya ukadiriaji kwenye hizi rasilimali. Kwa hiyo, itatoa zike double standards ambazo zilikuwa zinajitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri wakati akiwasilisha hapa, inaenda tena pia kutupa faida kubwa ya kuweka vizuri ule uthamini wa mali na kupatikana kwa haki za wananchi hasa wanavyopata fidia. Utakuja kuona pia kwamba inatoa fursa sasa ya kuwa na assessment nzuri za kodi na ninaamini Wizara na maeneo mbalimbali yataenda kupata kodi iliyostahiki huku ikiwaacha pia wananchi waweze kulipa kile ambacho wanastahili kulingana na sheria hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ambayo yalikuwa yanasumbua sana. Wananchi walio wengi wakati mwingine wamekuwa wakichelewa kupata mirathi kutokana na tatizo lililokuwepo. Sasa sheria hii inaenda kuondoa na kufanya urahisi wa kuweza kupata thamani hasa kwenye zoezi la usimamizi wa mirathi huko kwa wananchi wetu; lakini pia ku-facilitate zoezi la mauzo na manunuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa kilichokuwa kinanitia moyo, utaona lilikuwepo tatizo kubwa sana kwenye reporting framework ya hesabu zetu za upande wa Serikali. Utaona sasa hii inaenda kutibu, kwa sababu ukija kuangalia, siyo Tanzania tu, lakini nchi nyingi kuna tatizo la uthamini wa ardhi na nyumba, kuweza kuingia kwenye zile hesabu. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba huu ni mwanzo mzuri wa kuweza kufanya tuweze kuja kuwa na taarifa nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nimsahihishe kidogo msemaji aliyenitangulia kwamba tatizo la uthamini halijafika katika hatua hiyo katika Halmashauri zetu. Zoezi ambalo lilikuwa linafanyika kule alivyokuwa anzungumza hapa, hii ni stock taking, stock count ambayo ndiyo walikuwa wanafanya mara kwa mara, lakini walikuwa waniacha nje, zoezi la kuthamini mali kama vile ardhi pamoja na nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, unaona kabisa kwamba kupitia sheria hii, tunaenda ku-improve ile reporting framework kuanzia kwenye Halmashauri zetu na pia kwenye Serikali Kuu, vilevile kwenye ile consolidation ya national wealth.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, muswada huu ni muhimu sana, utarahisisha. Kwa sababu ukiuangalia kwa upana, unatoa nafasi sasa wale ma-valuer ambao tulikuwanao kuanzia kwenye ngazi ya Halmashauri, sasa wanaenda kuwa authorized valuers, kwa sababu walikuwa hawajapata ile nguvu ya kuweza kufanya kazi yao. Kwa hiyo, ninaamini kwamba tutaenda kuwa na improvement kubwa sana kwenye hesabu zetu. Yapo mambo mengi yanaonekana hapa na zoezi zima ata kuhusu watu kupata haki kupitia Bima, lakini pia kikubwa itaenda kusaidia kwenye soko letu la hisa, soko la mitaji. Kwa maana hiyo, kwamba tunapokuwa tumefanya uthamini kwa maana ya kwamba zile kampuni zitakapokuwa zinakwenda ku-deal na hii biashara kwenye soko la mitaji au soko la hisa, kwa hiyo sheria hii inaenda kuweka ubora zaidi katika ku-facilitate ili soko liweze kuwa effective. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka tu nichangie kwenye suala zimala muundo wa huyu Chief Valuer. Nafikiri la muhimu hapa ni upande wa Serikali kuangalia ni namna gani sasa huyu Chief Valuer kumwezesha aweze kufanya kazi vizuri. Kwa sababu utakuja kuona kwamba nilitaka nitofautiane na msemaji aliyetangulia kwamba, kumfanya Chief Valuer awe kama CAG. Ni kwa sababu Chief Valuer ana Bodi. Kwa hiyo, la muhimu ni kuifanya hii Bodi iweze kufanya kazi vizuri. Bodi hii ikiwezeshwa itamwezesha huyu Chief Valuer afanye kazi vizuri. Muhimu ni hicho kwamba tumwone sasa huyu Chief Valuer anaweza kufanya kazi yake kwa nguvu tuweze kuwa na mali yetu iweze kujulikana kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nikubaliane kwamba Chief Valuer huyu ni mtu ambaye atasimama kwenye nafasi yake, ataweza kusimamia sekta mbalimbali, ni cross-cutting. Kwa hiyo, ipo umuhimu tu wa Serikali kuitazama ofisi hii ili itakapoanza kufanya kazi zake aweze kufanya kazi kwa uzuri na kwa haraka zaidi ili tuweze kuondoa yale mambo ambayo tuliyaona kama ni shida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilitaka niseme kidogo kwamba nimevutiwa na kuwa na hii Bodi, kwa sababu utakuja kuona katika sehemu hii ya uthamini tunapokuwa na bodi; hii bodi ikifanya kazi kama tunavyoziona bodi nyingine kama NBAA, tumeona bodi inayoshughulikia hawa Maafisa wa Ununuzi, lakini tumeona pia hata kwenye upande wa sheria kwamba kabla watu hawajaenda ku-practice kipo chombo ambacho kinawa-regulate. Nimeona kwamba itakwenda vizuri kwa sababu inatoa fursa ya kwamba hawa wathamini kila wakati kuweza kufanya mitihani lakini pia ku-practice ili tuone kwamba wanaenda kufanya kazi nzuri. Utaona kabisa imeweka mamlaka ya bodi ili kuwa na labda na code of ethics, kuondoa ile hali ya uzembe. Kwa hiyo, yale yote ambayo yalikuwa yanaonekana kwamba kuna over valuation na under valuation yametajwa kwenye sheria hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona kabisa bodi hii inapewa fursa ya kusimamia miongozo mbalimbali ya ndani lakini pia miongozo ya Kimataifa. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba tumekuja sasa kuwa na chombo ambacho kitatufanya twende vizuri zaidi. Kwa hiyo, nataka niipongeze sana Serikali kwa kuja na sheria hii, lakini mimi ninaamini kabisa kuna mambo mengi yataenda kukaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho tu nilitaka nizungumzie pale kwenye usajili. Kwenye kile kifungu cha 26, ukikiangalia pamoja na kifungu cha 27, ili usajili wa hizi firm uzingatie kwamba mtu ambaye anaweza kwenda kusajili firm awe full registered, iwalazimishe hawa temporary registered na provisional ili waweze ku-team up na huyu ambaye yupo full registered ili firm ziweze kufanya vizuri. Nakushukuru kwa nafasi hii.
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Ardhini wa Mwaka 2018
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kusema naunga hoja zote hizi mbili zilizo mbele yako. Namshukuru pia Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu pamoja na Wajumbe, pia Waheshimiwa Wabunge ambao walihudhuria kwenye vikao vya Kamati na kutuboreshea Muswada huu. Nitazungumza mambo mawili tu; la kwanza nataka nizungumze upande ule wa ukaguzi hasa kwenye Muswada huu wa usafiri wa barabarani kwa maana ya kwamba ukaguzi ambao utafanywa na Mamlaka hii ya LATRA na lile suala la ukaguzi kupitia vyombo vyetu vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Muswada huu ni kudhibiti usafishaji barabarani kwa maana LATRA wata shughulika na suala la controls kwa maana kudhibiti na suala la Polisi kukagua magari barabarani wenyewe wanaangalia utekelezaji wa sheria maana yake compliance ya sheria wakiwa barabarani. Kwa hiyo hapa hakuna mwingiliano, kama ilivyo kwenye taaluma zingine ukiwa Daktari ukisha- graduate kuna Bodi ambayo inakutazama kwenye utekelezaji wa majukumu yako kama Daktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu madereva wameonekana kama ni watu ambao hawathaminiwi. Kwa maana hii sasa tunaichukua kama ni taaluma ili waweze kudhibitiwa. Tunajua kuwa na leseni ni jambo lingine lakini kuitumia vizuri kitaaluma leseni yako ni jambo ambalo LATRA wataenda kulitazama, kwa maana mtu awe na leseni lakini lazima tumwone pia anafanya kazi zake na kutufanya tuwe salama pia tukiwa huko barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka nizungumzie kuhusu mizani, kwamba sisi kama Serikali tumejipanga kuendelea kuboresha mizani zetu katika sehemu mbalimbali kwa maana ya kuzifanya ziwe za kisasa na kuzifanya zifanye kazi kwa tija na kufanya watumiaji wa barabara wasitumie muda mwingi wa kuwa barabarani, kwa sababu vituo vitakuwa vichache. Juhudi mbalimbali zinaendelea na kuna maeneo ambayo nafikiri Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla tunaendelea kufanya maboresho makubwa kwenye mizani zetu. Waheshimiwa Wabunge watakubaliana na mimi kwamba uko umuhimu wa kuzilinda barabara zetu na uwepo wa mizani hizi ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti na kuhakikisha barabara zetu ambazo tunatumia fedha nyingi kuzitengeneza zinabakia kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto ambazo zimekuwepo muda mrefu kwenye matumizi ya mizani barabani, lakini niseme tu Serikali imekuwa ikifanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba tunafanya maboresho na kuondoa changamoto ambazo muda mrefu zilikuwa zinatukabili huko barabarani. Kwa hiyo, nikuhakikishie na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumedhamiria kufanya ubora mkubwa katika udhibiti wa barabara zetu kwa kutumia mizani za kisasa, halafu kutakuwa na tija, usumbufu utakuwa mchache na watumiaji wa barabara hawatatumia muda mwingi watakapokuwa wakitumia barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo kwa sababu ya muda, nimalizie tena kwa kutoa shukrani kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja zote zilizoko mbele ya meza yako. Ahsante sana. (Makofi)