Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ezekiel Magolyo Maige (22 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba na mimi nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwanza kuwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Msalala kwa kunirudisha hapa kwa mara nyingine kwa kura nyingi. Imani yao kwangu nina uhakika italipa kwa sababu uwezo wa kuyatimiza niliyowaahidi kwa kushirikiana na Serikali hii ambayo iko vizuri sana ninaamini kwamba ninao.
Mheshimiwa Spika, naomba kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa ushindi mkubwa alioupata, lakini kipekee nimpongeze sana kwa hatua ambazo ameanza kuzichukua katika kurekebisha hali ya maisha ya Watanzania kupitia mpango wake wa kusaidia kwenye mambo mengi kama ambavyo amekuwa akiahidi.
Mheshimiwa Spika, Mheshiwa Rais, alituomba Watanzania tumuombee na mimi naomba kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba nimeweka mpango wa kuwa ninafunga angalau mara moja kila mwezi kwa ajili ya kumwombea Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake. Katika kumuombea nitakuwa pia nikimsaidia kupitia Serikali yake kuainisha maeneo ambayo majipu yapo katika hatua nzuri ili yaweze kushughulikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliainisha mambo mengi lakini ukurasa wa nane alisema ifuatavyo naomba ninukuu kwamba; “Suala la madini nalo limelalamikiwa, wanalalamika wenyeji kutofaidika, vilio vya wachimbaji wadogo wadogo kutengewa maeneo ya uchimbaji na kupatiwa mikopo, kutolipa kodi stahiki, usumbufu wa kulipa fidia na kadhalika.”
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo naomba nijikite kwenye hili eneo, Wilaya ya Kahama tuna migodi miwili, Mgodi wa Bulyanhulu na Mgodi wa Buzwagi. Eneo hili ni chanzo kikubwa sana cha mapato kwa Serikali na ni chanzo kikubwa cha mapato kwa wananchi ambao wanazunguka migodi hiyo. Tumekuwa tukilalamika kila wakati, niipongeze Serikali ya awamu iliyopita ya Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa hatua ambazo ilichukua kurekebisha mikataba. Itakumbukwa aliunda Tume iliyoongozwa na Jaji Mark Bomani, mimi na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge akiwemo Mheshimiwa Waziri Mwakyembe tulikuwa Wajumbe na kupitia Tume hiyo kulifanyika mabadiliko kadhaa ambayo yamepelekea kuongezeka kwa mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba niiombe Serikali, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Pofesa Muhongo kwa hatua ambazo ameanza kuchukua kutusaidia kwenye eneo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukilalamika kwamba wananchi wa maeneo ya migodi hatunufaiki na madini, kwanza kwa sababu migodi hii hailipi kodi sawasawa kwenye Halmashauri, lakini pili, procurement zake nyingi wamekuwa wakinunua vifaa vingi kutoka maeneo ya mbali ya migodi na mbaya zaidi miradi ya ujirani mwema, wamekuwa wakichangia kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka mwaka 2014 Mheshimiwa Profesa Muhongo alisimamia mazungumzo baina ya Mgodi na Serikali kwa upande mmoja lakini na sisi wananchi wa maeneo jirani hatimaye Mgodi wa Bulyanhulu, Buzwagi na mingine wakakubali kuanza kulipa ushuru wa huduma kwa Halmashauri kwa asilimia 0.3. Hatua hiyo imesaidia kuongeza mapato ya Halmashauri lakini kama ambavyo Mheshimiwa Waziri utakumbuka katika mazungumzo yale tulikufahamisha, tunaomba uendelee kutusaidia. Hawa jamaa ni jeuri, na utakumbuka katika mazungumzo kuna baadhi ya mambo waliyakubali lakini utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua kwa mfano walisema watakuwa wanalipa hiyo service levy kila robo mwaka, sasa hivi inafika mpaka nusu mwaka hawajalipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baya zaidi, tulisema kwamba kwa mfano Mgodi wa wa Bulyanhulu umeanza uzalishaji mwaka 2000 na toka wakati huo hawajawahi kuzalisha dhahabu ya chini ya thamani ya dola za Kimarekani milioni 500, ukipiga hesabu ya asilimia 0.3 ya dola milioni 500 ni fedha nyingi sana. Kwa hesabu nilizofanya Halmashauri ya Wilaya ya Msasala inapaswa katika kipindi hicho cha miaka 15 iwe imelipwa kutoka Mgodi wa Bulyanhulu dola za Kimarekani zisizopungua milioni 13 hivi sasa wanatulipa milioni 700, milioni 600 ambazo ni kidogo kuliko tunavyotaka.
Mheshimiwa Waziri, naiomba Serikali kusaidia kama ambavyo tulikuwa tumeanzia, mtusaidie tulipwe madeni yetu dola milioni 12 tunazodai Mgodi wa Bulyanhulu ambayo ni 0.3% kutoa dola 200,000 ambazo wamekua wakilipa, ile difference ile toka mwaka 2000 ni karibu dola milioni 12, fedha hizo zikilipwa ninaamini kwamba maisha ya wananchi yataboreka sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, naomba nimwombe Waziri atusaidie sana katika utekelezaji wa miradi ya ujirani mwema hawa watu wamekuwa hawana imani na Taasisi za Serikali, wamekuwa wakiitekeleza wao wenyewe na kwa mara nyingi wamekuwa wakitekeleza miradi kwa gharama kubwa, kwa mfano, wametujengea kituo cha afya pale Bugalama kwa thamani ya shilingi milioni 850.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zile zingetolewa kwenye Halmashauri, tukajenga sisi kama ambavyo tunajenga miradi mingine milioni 850 tungemaliza kujenga angalau majengo mengi zaidi yenye uwezo wa ku-accomodate hata huduma za kihospitali yenye hadhi ya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba, Mheshimiwa Waziri atusaidie mazungumzo ambayo bado yanaendelea kati yetu na wawekezaji hawa waweze kuziamini Taasisi za Serikali, waiamini Halmshauri ili wanapotekeleza miradi ya ujirani mwema kwa kiasi kikubwa itekelezwe kwa modality ambayo Halmashauri yenyewe itasimamia, na kwa kufanya hivyo tutaweza kupata value for money.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi tatizo la sheria ya manunuzi ambalo tunalilalamikia Serikali, kule mgodini ndiyo liko kubwa zaidi, kwa sababu unakuta shule ambayo ingeweza kujengwa kwa milioni 50, milioni 80, wao wanasema wamejenga kwa milioni 300, milioni 400. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo katika mazunguzo hayo tumekuwa na kilio cha wananchi waliondolewa kwenye eneo la Mgodi wa Bulyanhulu mwaka 1996. Waliondolewa bila fidia, tumefanya mazungumzo haya kupitia awamu iliyopita na Mawaziri kadhaa, Profesa Muhongo ulianza kuchukua hatua nzuri za kukaa chini kuzungumza na hawa watu niombe katika mazungumzo ambayo umekua nayo, na nipongeze sana jitihada ambazo umekuwa ukizifanya na nimshukuru Mungu kwa kurudishwa kwenye hii Wizara. Kwa sababu institutional memory imekuwepo, haya ninayoyasema unayajua, naamini kwamba utatusaidia tuzungumze waweze kulipa fidia kwa wananchi waliokuwa waki-occupy lile eneo ambao waliondolewa mwaka 1996 bila fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dakika chache zilizobaki naomba Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi anisikilize vizuri. Kuna tatizo la Mwakata tulipata maafa tarehe 3 Machi, mwaka jana watu 47 wakafa, wananchi kaya zaidi ya 650 zikakosa makazi, Waziri Mkuu akaja, Rais akaja, na mkaahidi kwamba mngesaidia kujenga nyumba mia tatu na kitu. Mpaka leo hii wale watu wanaishi kwenye maturubai, hizi mvua zinazonyesha zinawanyeshea, ni kitu ambacho hakiaminiki kabisa kwa sababu Serikali ilikuwa inaahidi na kwamba tulitegemea jambo hili lingetekelezwa kwa dharura katika kipindi cha mwezi mmoja, miwili na ndiyo maana ya kuwapa maturubai.
Leo, wale watu wanakaa kama wakambizi, nyumba zilizojengwa ni tatu ambazo zimetoka kwa wafadhili wa Mgodi wa Bulyanhulu pamoja na wafadhili wengine. Msaada au ahadi iliyotolewa na Rais kwamba nyumba zile zingejengwa hakuna kilichofanyika hata kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kasi ambayo Mheshimiwa Rais anayo, ninaomba sana Mheshimiwa Jenista, baada ya hapa hatua inayofuata ni kufuatana na mimi tena twende mapema iwezekanavyo. Twende pale Mwakata, eeh Mheshimiwa Mwamoto anasema na yeye awepo kwenye msafara huo, twende Mwakata ukawaeleze wananchi ni nini na lini nyumba hizo zitajengwa. Wale wananchi wanaishi maisha ya kisikitisha sana kwa sababu hawana nyumba na wanamatumaini ya kujengewa nyumba na Serikali yao, na ninaamini Serikali yetu sikivu itaweza kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la mwisho, ni ahadi ya kupeleka maji kwenye Mji mdogo wa Isaka pamoja na Mji mdogo wa Kagongwa na baadae yaende hadi Tinde. Hii ni ahadi iliyotolewa na Serikali iliyopita toka mwaka 2008, najua limekuwepo tatizo la fedha lakini tumekuwa tukiahidiwa kila wakati nakumbuka kwenye Bunge lililopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nitazungumza tena siku nyingine. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie bajeti hii ya Wizara ya Biashara. Naomba nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kuwa hivi nilivyo leo. Kipekee niwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Msalala kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa wananchi hawa wa Jimbo langu la Msalala wamenipa nafasi kwa mara nyingine ya kuja kuwawakilisha hapa Bungeni, wamenipa heshima kubwa, naamini nitaitumia vizuri …
Kwa ajili ya maslahi na maendeleo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na timu yake ambayo kwa kweli dhahiri kazi inayofanyika kila Mtanzania anaikubali.
Mimi naamini kampeni nzuri inafanywa na Serikali yetu kupitia matendo ambayo yanafanywa na kwa maana hiyo wana-CCM wenzangu wala tusipate hofu mwaka 2020 kama siyo robo basi watakuwa wamebaki theluthi au watakuwa wamepungua zaidi kwa sababu kazi inafanyika vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa rafiki yangu sana Waziri wa Viwanda. Hotuba yake imesheheni matumaini makubwa sana. Kwa kweli naamini, endapo nia ya Waziri itatekelezwa kama ambavyo mwenyewe anatamani tutafika kwenye nchi ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimsaidie Mheshimiwa Waziri baadhi ya maeneo ambayo yanaweza kumsaidia sana. Cha kwanza naomba ufahamu kwamba Wizara yake ni kiungo. Serikali kwa miaka mingi ilishajitoa kwenye uzalishaji na kwenye biashara moja kwa moja. Serikali haijengi viwanda, haina mashamba, haifanyi chochote zaidi ya kuweka mazingira mazuri kwa biashara kufanyika. Ili biashara ziweze kufanyika cha kwanza ni muhimu kuangalia mazingira yanayoweza yakaruhusu biashara hizi kushamiri. Ili tuweze kufika huko, nikuombe Mheshimiwa Waziri rejea kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais alipolihutubia Bunge tarehe 20 Novemba, 2015, alituwekea dira kwamba anapenda ndani ya miaka mitano hii asilimia 40 ya ajira zitokane na viwanda. Ni suala kubwa ambalo nilitegemea kwenye hotuba yako kwa kiasi fulani ungeweza kuwa umeligusia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nini kinachopaswa kufanyika kwenye eneo hili ambacho sijakisikia, ninachosikia tu ni kwamba tutakuwa na viwanda na kadhalika.
Nilipenda kupitia kauli hiyo ya Mheshimiwa Rais Waziri atufanyie study na atuletee ili nasi tuweze kuwa tunafuatilia na kumshauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza, ni vizuri angeweza kutupa baseline data kwamba hivi sasa ajira zilizopo ni kiasi gani na zinazalishwa ngapi kwa mwaka. Kati ya hizo ajira kiasi gani au asilimia ngapi inatokana na viwanda. Akishapata hiyo takwimu atuambie mwaka 2020, 40% ya ajira zote zitatokana na viwanda maana yake tutakuwa na ajira ngapi zitakazotokana na viwanda. Ili kufika huko aende mbele zaidi ajaribu kuangalia ni sekta zipi zinaweza zikampa hizo ajira zinazohitajika na kuzitazama hizo sekta ni vizuri pia akaangali ni vitu gani vya kufanya katika sekta hizo. Eneo mojawapo la muhimu la kuliangalia ni mazingira ya kodi, upatikanaji wa malighafi pia aina na upatikanaji wa wafanyakazi watakaofanya kazi kwenye hivyo viwanda na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la malighafi ambalo mimi naliona ni muhimu sana hakuna eneo litakalotoa malighafi nyingi za ku-feed viwanda vyetu zaidi ya eneo ambalo rafiki yako na rafiki yangu na mdogo wangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba analisimamia, Wizara ya Kilimo. Wizara hii ya Kilimo ni Wizara pacha na Wizara hii, naomba mfanye kazi kwa pamoja. Sekta hii Mheshimiwa Waziri itakupa 95% ya malighafi zote unazohitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano wa eneo moja, malighafi moja muhimu na kubwa inayoweza ikasaidia viwanda ni inayotokana na zao la pamba. Pamba inatoa nyuzi, nguo, mafuta, mashudu yanayotumika kulishia mifugo na vitu vingi ambavyo vyote vinakwenda kutumika kwenye viwanda. Angalia hali ya zao hili ambalo ndiyo malighafi muhimu kwa viwanda unavyohitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1995 pamba tuliyozalisha nchini ilikuwa zaidi ya tani 600,000. Kwa takwimu za Mheshimwia Mwigulu ambazo alizisoma hapa juzi mwaka 2014/2015 tumezalisha pamba tani 245,000 na tunategemea mwaka 2016 tutazalisha pamba tani 145,000 ina maana uzalishaji wa pamba umeshuka kutoka tani 600,000 miaka mitano iliyopita au kama siyo mitano ni kumi hadi wastani wa tani 150,000. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini uzalishaji wa zao la pamba umeanguka? Kama uzalishaji wa pamba unaendelea kuanguka maana yake hautapata malighafi na bila malighafi maana yake hautapata viwanda na usipopata viwanda, ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kufikia 40% ya ajira zitokane na viwanda haitatimia. Kuna nini kwenye pamba? Yapo matatizo mengi, kaeni na Mheshimiwa Mwigulu mshirikiane kupata majibu ya msingi ya matatizo ya eneo hili. (Makofi)
Mheshimwia Naibu Spika, matatizo wanayokabiliana nayo wakulima wa pamba moja ni bei inayoratibiwa na soko la dunia. Ni lazima tutafute namna ya kupambana na tatizo la bei. Tuliwahi kupendekeza hapa kwamba ni vizuri tukaanzisha mfuko wa ku-stabilize bei ya pamba (price stabilization fund) ya pamba ili pale bei inapoanguka kwenye soko la duni mkulima aweze kupata fidia. Ni wapi suala hili limefikia? Kaeni na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo mpate namna ya kutatua tatizo hili. (Makofi)
Mhehimiwa Naibu Spika, tatizo la pili linalojitokeza ni suala la dawa. Mwaka huu tumeletewa dawa inaitwa “ninja” haiuwi wadudu. Kimsingi kilichofanyika ni wizi, ni uhujumu uchumi. Mheshimiwa Mwigulu nakufahamu, nakuamini, naomba ufahamu kwamba mwaka huu pamba uzalishaji utakuwa chini ya nusu ya ile uliyotarajia kwa sababu dawa iliyoletwa hii inayoitwa “ninja” haiuwi kabisa wadudu badala yake wadudu wanafurahia kuwa kwenye maji maji ya ile dawa kwa sababu yanawapunguzia joto. Wanakula vizuri zaidi yale matunda ya pamba na pamba haikomai. Kwa hiyo, suala la dawa ya “ninja” naomba tupate taarifa ni nani aliye-supply na kwa nini haiui na hatua gani zinachukuliwa kwenye jambo hili ambalo ni uhujumu uchumi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala la mizani kwenye pamba. Kwa kawaida ninavyojua mimi ni kwamba unapoenda kuuza kitu anayemiliki mizani ni yule muuzaji. Ukienda kwa mtu anayeuza sukari mzani utaukuta kwa muuza sukari, ukienda kwa mtu anayeuza kitu kingine chochote hata petrol station mzani au pump iko kwa muuzaji. Kwa zao la pamba pump au mizani anayo mnunuzi au wakala wake, jambo hili si sawa. Katika mazingira hayo, wanachezea mizani, tulianza na ile mizani ya ruler ikawa haitumiki, sasa hivi wanatumia mizani ya digital ndiyo wanaharibu kabisa wanawaibia wakulima wa pamba. Naomba shirikianeni hizi Wizara mbili mpate ufumbuzi wa tatizo la mizani ya pamba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine kwenye suala hili la pamba ni kodi kwenye mafuta ambayo yanatokana na pamba hasa VAT ambayo inawanyima nafasi ya kushindana na mafuta yanayotoka nje lakini kubwa na mafuta yanayozalishwa na viwanda vingine. Kwa mfano, pale Shinyanga kuna kiwanda cha Mchina ambacho kimewekwa kwenye mazingira ya uwekezaji ya EPZ, amesamehewa kodi nyingi, wakulima wa kawaida na wenye viwanda vidogo vidogo vingine vya ukamuaji wa mafuta ya pamba hawana misamaha hiyo, kwa hiyo mafuta wanayozalisha wanashindwa kushindana naye. Niombe eneo hili nalo mlirekebishe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine hata yale mashudu wanayozalisha kutoka kwenye makapi yanayotokana na matunda ya pamba nayo yanatozwa VAT. Mimi navyojua mali zote au vitu vyote vinavyotumika kwa ajili ya kuendeleza mifugo vinapaswa kusamehewa kodi. Mashudu yanayotokana na pamba yanatozwa VAT matokeo yake wafugaji wanashindwa kuyanunua na kunenepesha mifugo yao. Niombe Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Waziri Viwanda na Biashara shirikianeni kupata ufumbuzi, hizi kodi ambazo kimsingi wala hazina maana yoyote zaidi ya kuleta bugudha kwa wakulima na wafugaji ziweze kuondolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuomba sana, Mheshimiwa Waziri kaa na wafanyabiashara, watakusaidia sana. Kwa kuwa wewe huwezi ukajenga viwanda basi ukae nao watakueleza wana matatizo makubwa ya jinsi kodi zinavyokokotolewa, wana matatizo makubwa jinsi wanavyopata malighafi, wana matatizo makubwa jinsi wafanyakazi wanaoajiriwa kwenye viwanda vyao wanavyo-behave. Sheria ya Kazi na Mahusiano Kazini kwa kiasi kikubwa inajenga mazingira ya wafanyakazi kutofanya vizuri kama ambavyo wawekezaji wanapenda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, naomba kusema kwamba naunga mkono sana hoja hii, namshauri Mheshimiwa Waziri aondoe vikwazo kwenye upatikanaji wa malighafi. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwanza kwa ushindi mkubwa alioupata lakini kwa kazi kubwa anazofanya hadi hivi sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hayo, moja ya eneo kubwa ambalo limekuwa likileta shida sana katika mambo ambayo sisi wana-CCM tumekuwa tukiahidi ni utengaji wa fedha kwa ajili ya sekta ya miundombinu. Kwa mara ya kwanza Mheshimiwa Rais amekuwa kwenye ofisi hiyo na tumeshuhudia shilingi trilioni zaidi ya nne zimetengwa kwa ajili ya miundombinu. Naomba nimpongeze sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, naomba nionyeshe masikitiko yangu kwenye baadhi ya maeneo. Baadhi ya Wabunge wamezungumzia, ninaamini kwamba fedha hizi zingeweza kufanya kazi nzuri sana katika utekelezaji wa Ilani yetu ya CCM, lakini ninavyoona kuna hatari kubwa ya kutapanya fedha hizi kwenye maeneo mengi na mengine ambayo wala hayaendani kwa kiasi kikubwa na Vision 2020 - 2025 na mengine wala hayawiani na ahadi ambazo tulizitoa kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la reli. Reli ya kati iko katika Ilani ya CCM, ukisoma Ilani yetu tuliahidi ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge. Si kwamba tutaanza, si kwamba tutafanya feasibility study au tutafanya kitu kingine chochote. Mimi kama Mwenyekiti wa Wabunge wanaotoka kwenye ukanda unaopitiwa na reli ya kati, tumekuwa na mazungumzo kwa nyakati kadhaa na Mheshimiwa Waziri tukizungumzia suala hili na hata tunapokuja kwenye bajeti yake tulikuwa hatujakutana kuzungumza na kuweka mkakati na Wabunge wenzangu kwa sababu Mheshimiwa Waziri amekuwa akituhakikishia mipango aliyoweka kwenye bajeti yake itahakikisha reli inajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kusema kwamba Waziri ametu-betray kwa sababu upembuzi yakinifu na mambo mengine ya awali kabla ya ujenzi kuanza yalikuwa yameshakamilika na tulichokuwa tunategemea kwa hatua ya sasa ni kutafuta fedha na kuanza kujenga. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote ambao tunatumia reli ya kati, ambao wananchi wetu wanaumia kimaisha kutokana na ughali wa bidhaa zote tuliangalie suala hili. Kwa mfano, mabati, nondo, cement zote zinatoka Ukanda wa Pwani, viwanda vyote vya cement viko Ukanda wa Pwani lakini ujenzi unafanyika mpaka Kigoma. Mfuko wa cement Kigoma ni zaidi ya shilingi 20,000/=, mfuko wa cement Dar es Salaam ni shilingi 12,000/=, shilingi 8,000 anayolipa mwananchi wa Kigoma ni adhabu anayopewa kwa sababu tu Mheshimiwa Waziri hajachukuwa hatua za kujenga reli ya kati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hatua hazichakuliwa kwa sababu ukisoma ukurasa, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuchukuwe vitabu vya hotuba ya Waziri, muangalie ukurasa wa 72, ile Iibara ya 127. Ukisoma ile ibara inasema, mpango uliokuwepo mwanzo ulikuwa ni wa kujenga reli kwanza kwa kujenga sisi wenyewe lakini pia kwa kutumia mpango wa PPP, Serikali imiliki reli, sekta binafisi iendeshe. Waziri anasema mpango huo umekwama na sasa wamefuta mwezi Februari baada ya kukutana na Mawaziri wenzake wa Rwanda na Burundi sijui wanachangia shilingi ngapi katika ujenzi wa reli ya kwenda Mwanza, mbaya zaidi wamefuta na sasa wanasema utajengwa kwa utaratibu mwingine unaitwa Sanifu, Jenga, Endesha, Kabidhi. Utaratibu huu utaanzia kwenye design ambayo inaonyesha kwamba itakamilika baada ya miezi 24. Ukihesabu miezi 24 kuanzia sasa obvious itakwenda zaidi ya mwaka 2019 na ilani yetu ya CCM ilisema tutajenga reli kabla ya mwaka 2020, tutakuwa tumeiba kura za wananchi kwa kuahidi reli ambayo haitakuwepo. (Mkaofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara ya kwanza naomba niseme maelezo ya Waziri hayajaniridhisha kwenye suala hili. Kwa maana hiyo nilikuwa naomba endapo Waziri katika majumuisho yake hatasema ni nini kitafanyika kuanza kujenga reli wala siyo maneno yaliyoko kwenye ukurasa wa 72 nilioonyesha, mimi binafisi na Wabunge wenzangu nitawashawishi sana wote tunaotumia reli ya kati tusikubaliane na jambo hili hadi tutakapohakikisha reli inajengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siko tayari mimi kuhukumiwa kwa kuiba kura, nimesimama Isaka niwaambia reli inajengwa sikuwaambia kwamba tunaanza kujenga kwa utaratibu tofauti, sikuwaambia kwamba tunaanza upembuzi yakinifu, tulisema tunaanza kujenga reli. Naomba reli ijengwe, bila kufanya hivyo Wabunge wote tunachimbiwa shimo, Mheshimiwa Mwakasaka hutarudi na rafiki zangu wote hamtarudi kwa sababu reli haitajengwa na hata Mheshimiwa Genzabuke hautarudi. Mpango wa ujenzi wa reli hauridhishi na hauendani na ahadi tulizotoa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia suala hilo, naomba nizungumzie suala lingine la barabara na hapa nizungumzie barabara yangu ambayo kimsingi inakidhi vigezo vyote. Mbunge mmoja amesema kwamba tunataka barabara zinazounganisha mikoa na mikoa ndipo twende kwenye barabara zinazounganisha wilaya na wilaya na baadaye kata na kata. Wote ni Watanzania na wote tunalipa kodi, tumekuwa tukizungumza toka mimi nimekuwa Mbunge mwaka 2005 kuunganisha mkoa wa Shinyanga na Geita. Tunasema kuunganisha, kwanza ni kuunganisha mkoa na mkoa lakini baya zaidi maeneo haya yana uchumi mkubwa unaoendesha uchumi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kahama kuna migodi miwili, Mgodi wa Bulyanhulu na Mgodi wa Buzwagi, Geita kuna Mgodi wa Geita. Si mara moja wala mara mbili mimi nimezungumza na wenye migodi ile na bahati mbaya kanuni haziruhusu lakini ningeomba kama utaruhusu tutengue kanuni tumkaribishe Injinia Dabalize aliyekuwa Mhandisi wa TANROADS Mkoa wa Shinyanga, tulishazungumza na watu wa Mgodi wa Bulyanhulu, tulishazungumza na watu wa Mgodi wa Geita wanasema wako tayari kushiriki katika ujenzi wa barabara ya Kahama - Geita kwa kiwango cha lami, upembuzi yakinifu umeshakamilika. Kwenye hotuba ya Waziri barabara hiyo wala haijatajwa, wala hajaonyesha nia yoyote ya kuzungumza na hawa wawekezaji ambao wako tayari kushiriki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kahama, Msalala, Geita siyo kwamba tu wanahitaji barabara hiyo kwa sababu ya umuhimu wake wa kibiashara lakini wanahitaji pia kwa sababu ya masuala mazima ya afya.
Waheshimiwa Wabunge wenzangu hii barabara kwa wale ambao hamjaipitia, inapitisha malori yenye kusomba mafuta kupeleka mgodi wa Bulyanhulu, inapitisha malori yanayosomba mchanga wa dhahabu kutoka mgodi wa Bulyanhulu kwenda nje ya nchi na kwa wastani kwa siku zinapita semi trailer zaidi ya 200. TANROADS Shinyanga na Geita wamejaribu kuwa wanakarabati barabara hii lakini haiishi zaidi ya miezi miwili imeshaharibika. Sasa niulize, hivi nini kinakwamisha kuanza ujenzi wa barabara hiyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri sana Mheshimiwa Rais ambaye alikuwa Waziri wa Ujenzi miaka ya nyuma, alisema na akahakikisha kwamba barabara hii itaanza kujengwa immediately baada ya kuwa ameshaingia madarakani kama Rais.
Ninaamini jambo hili Mheshimiwa Rais halifahamu na naomba Mheshimiwa Rais huko uliko ufahamu kwamba Mheshimiwa Profesa Mbarawa hajaanza kuweka mpango wa kujenga barabara ya Kahama - Geita kama ulivyoahidi ulivyokuwa unahutubia wananchi wa Kahama. Ninaamini amefanya hivyo kinyume cha dhamira yako, kinyume cha matakwa ya Watanzania wanaoishi Kahama na Geita. Naomba Mheshimiwa Waziri tafuta fedha ujenge hii barabara, upembuzi yakinifu umekamilika, wawekezaji wa hiyo migodi wako tayari kuchangia ili mradi Serikali ikubaliane nao namna ya kurekebisha masuala ya kodi, kufanya tax rebate kwa miaka ya mbele kutokana na uchangiaji watakaokuwa wamefanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimepigiwa kengele nimalizie kwa kuomba sana kwamba Kanda ya Ziwa tunategemea uwanja wa ndege wa Mwanza uwe wa Kimataifa kwani utafungua ukanda wetu ule ili tuweze kupata watalii. Nimeona kuna fedha zimetengwa lakini ningeomba tu Waziri atuambie hivi ni lini uwanja wa ndege wa Mwanza utakamilika kujengwa kwa kiwango cha kimataifa na utakuwa International Airport ili wageni waingilie uwanja wa ndege wa Mwanza, waingie Serengeti watokee KIA au waingilie KIA waje watokee Mwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naona bado kuna dakika chache, nimalizie kwa kusema jambo lingine kwamba ili kupunguza msongamano wa malori Dar es Salaam kumekuwepo na pendekezo la kuweka dry port nje ya Dar es Salaam hasa eneo la Kibaha. Naomba Wizara hii ilichukulie jambo hili kwa uzito unaostahili, tujenge bandari kavu eneo la Kibaha ili malori yasiwe yanaingia Dar es Salaam hasa kwa kuangalia misongamano na ajali zinazotokea ambazo kwa kwa kweli hazina maana yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Niombe kwa dakika chache zilizobaki feasibility study ya barabara ya kutoka Kahama - Mwanza kupitia Bulige na Solwa ianze. Feasibility study ya barabara ya kutoka Kahama - Msalala - Nyang‟hwale - Busisi ianze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Mheshimiwa Rais na Makamu wa Rais walipokuja Nyang‟hwale pale kwenye mkutano Karumwa waliahidi barabara ya kutoka Busisi - Sengerema - Nyang‟hwale – Karumwa - Msalala - Kahama nayo itajengwa kwa kiwango cha lami. Ni barabara inayounganisha mikoa mitatu na ina sifa zote za kujengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na mimi nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kutuwasilishia Mpango ambao sisi kama Wabunge tuna wajibu wa Kikatiba wa kutoa maoni yetu ili kuuboresha ili uweze kuwa na manufaa makubwa kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla Mpango ni mzuri sana na kwa kweli nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa sababu yako baadhi ya maeneo ambayo tumekuwa tukiyazungumza sana ameyataja japo si kwa kiwango kikubwa ambacho tungetarajia lakini walau yamezungumzwa. Mojawapo ni suala la uboreshaji na ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kwenye Bunge lililopita tulizungumza sana eneo hili, tulikasirishana sana na moja ya eneo tulilokuwa na wasiwasi ni ujenzi wa reli hii kwa kiwango cha standard gauge kwenye matawi yake yote. Nashukuru kwenye Mpango liko wazi, matawi yote yametajwa Kaliua - Mpanda - Karema - Uvinza - Msongati - Isaka - Keza na sehemu zingine. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, eneo hili ni la muhimu sana, tunakubaliana na yeye na yako maeneo mengi ambayo tunakubaliana. Naamini kwamba tukienda kutekeleza matokeo makubwa tutayapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama taratibu zinavyotaka nifanye, naomba nizungumzie baadhi ya maeneo ambayo naamini yanaweza yakasaidia zaidi kufanya Mpango uweze kuwa na manufaa makubwa kwa wananchi lakini lengo kuu likiwa ni kutusaidia katika kufikisha au kutekeleza ahadi tulizozitoa. Kwenye kitabu cha Mapendekezo ya Mpango ukurasa wa 62 Mheshimwa Waziri ameeleza maeneo ya kipaumbele kwa mwaka 2017/2018. Kwenye maeneo hayo yako baadhi ya maeneo ambayo mimi naamini yalitakiwa yaingizwe na yangefaa yatizamwe kwa upana mkubwa sana. Eneo moja ambalo mimi naona halijaelezwa kwa upana unaostahili ni mchango wa sekta ya kilimo kwa upana wake kama engine ya raw material inayotakiwa kwa ajili ya uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba hauwezi ukajenga viwanda bila malighafi na asilimia zaidi ya 80 ya malighafi zinazohitajika kwenye viwanda zinatoka kwenye sekta ya kilimo. Ili kweli kupata uchumi wa viwanda ni lazima tuangalie maeneo ya sekta ya kilimo na hasa mazao ambayo kwanza yanaajiri watu wengi lakini pili yana multiplier effect kubwa mfano ni zao la pamba. Zao la pamba mwaka 2000 tulizalisha marobota kama milioni moja na laki mbili hivi, uzalishaji wa mwaka jana ilikuwa ni chini ya marobota laki mbili. Kuzalishwa kwa pamba kwa kiwango kidogo namna hiyo kwa lugha rahisi maana yake ni kwamba zao la pamba limeanguka. Kuanguka kwa zao la pamba kunamaanisha wananchi wanaofikia zaidi ya milioni 14, wananchi wanaotoka kwenye Wilaya zaidi ya 42 ambao kwa kiasi kikubwa shughuli zao za kiuchumi zimekuwa zikitegemea pamba hawana shughuli ya kufanya. Iko Mikoa ambayo hauwezi ukapambana na umaskini kwenye mikoa hiyo bila kugusa pamba, mojawapo ni Mkoa wa Shinyanga na Simiyu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwenye mpango huu, mkakati maalum wa kufufua sekta ya kilimo utajwe, acha tu kutaja kwa ujumla jumla kwamba kuongeza pembejeo, lakini uwepo mkakati maalum wa kufufua zao la pamba, kujenga viwanda vya mafuta yanayotokana na mbegu za pamba vilevile viwanda vya kusokota nyuzi za pamba na hatimaye kupata nguo. Tukifanya hivyo, tutatoa ajira kwa Watanzania zaidi ya milioni 14 lakini pia tutaondoa umaskini kwa mikoa zaidi na nane ambayo inaishi kwa kutegemea zao la pamba. Kwa hiyo, eneo hili nilidhani ni muhimu Mheshimiwa Waziri akalitizama kwa umakini unaostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni zao la mifugo na hapa kuna tatizo kubwa sana. Hivi sasa tunakisiwa kuwa na ng‟ombe, mbuzi na kondoo zaidi ya milioni 26. Mifugo hii wote tunajua ambavyo imekuwa ni kero kati ya wahifadhi na wakulima kwa upande mmoja pamoja na mifugo yenyewe. Ukiangalia kinachopatikana kutoka kwenye mifugo hii kimsingi ni kama hakihesabiki (negligible). Naiomba sana Wizara hasa Wizara ya Fedha pamoja na Wizara ya Kilimo mkae pamoja muwe na mpango mkubwa pia wa ujenzi wa viwanda vya nyama, ujenzi wa viwanda vya maziwa, ujenzi wa viwanda vya ngozi, tuache hivi viwanda vidogo vidogo ambavyo vimekuwa vikisemwa na rafiki yangu mmoja ametajwa hata hapa Waziri wa Viwanda kwamba anachukulia suala la viwanda ni suala rahisi, ni suala ambalo ni complicated sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani ng‟ombe hawa zaidi ya milioni 25 ambao kwa wastani wa bei ya soko ya shilingi 300,000 kwa ng‟ombe mmoja unazungumzia utajiri wa zaidi ya shilingi trilioni 7.5, ambayo ni karibia theluthi moja ya bajeti yetu ya Serikali, utajiri wa namna hiyo tunauona hauna thamani, wafugaji tunawafukuza kila mahali na kuwaambia warudi walikotoka. Mimi nimekuwa nikihoji sana hiyo lugha ya kusema watoke kwenye hifadhi warudi walikotoka, nikawa najiuliza hivi sisi Watanzania tukiambiwa turudi tulikotoka itakuwaje? Kwa sababu Watanzania tulio wengi wengine wana asili ya Asia, wengine Wabantu wana asili ya Afrika ya Kati na wengine Nilotics wana asili ya Afrika ya Kaskazini, hivi na sisi turudi huko? Ni lazima tujue mifugo ni rasilimali yetu tuiwekee mkakati maaalum mzuri wa kuiendeleza wala si kuiona kwamba ni kero na inawezekana. Kwa hiyo, naomba sana eneo hili la mifugo liweze kutazamwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni la mtawanyiko wa uwekezaji wa kimkakati katika nchi. Kuna eneo ambalo tumezungumzia miradi ya kielelezo na kanda za kiuchumi, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 18. Ukitazama kanda za kiuchumi zilizotajwa za Pwani, Tanga, Dar es Salaam, Mtwara na Kigoma, najiuliza kama kweli tunataka kufanya kanda ya mkakati wa kiuchumi iwe kanda hiyo na huko ndipo pengine tutakoweka uwekezaji mkubwa na biashara kubwa na viwanda, haitawezekana kwa malighafi zitakazotoka katikati ya nchi yetu za mifugo na mazao ya kilimo kuyapeleka kwenda kuchakatwa kwenye viwanda ambavyo vitajengwa maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ukuzaji wa uchumi kwa kanda za kiuchumi za kitaifa ziwe kijiografia kwa kuangalia kila eneo linazalisha nini? Tuwe na makakati maalum wa kuendeleza mifugo kwa hiyo tuwe na kanda maalum ya Dodoma; Kanda ya Mwanza tuwe na mkakati maalum wa kuendeleza madini, kuendeleza kilimo cha pamba na kuendeleza mifugo. Kanda ya Kigoma kule kwa kina Nswazugwako tuwe na mikakati hiyo ya kuendeleza uvuvi wa Lake Tanganyika, mawese na vitu kama hivyo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inatofautiana utajiri wa rasilimali eneo kwa eneo, hauwezi ukategemea chuma cha Liganga kiwe rasilimali kwa kiwanda kitakachojengwa Tanga au kiwanda kitakachojengwa Bagamoyo. Kwa hiyo, ni lazima eneo ambalo rasilimali inapatikana, mifugo inapatika Shinyanga kiwanda cha nyama kijengwe huko na ndiyo huko kuufanya uchumi uweze kugusa Watanzania wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie eneo moja ambalo naona kama linasahaulika la misitu. Uzalishaji wetu na potential yetu kwenye misitu hatuitumii vizuri. Bahati mbaya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili hayupo, nchi ya Finland kwa mfano, uchumi wake zaidi ya Euro bilioni 20 kwa mwaka unatokana na mazao ya misitu. Ardhi wanayolima ni kama hekta milioni mbili, sisi ardhi yetu iliyoko kwenye hifadhi (forest reserves) ni hekta milioni 13 na eneo linalolimwa kwa maana ya forest plantation ni hekta 80,000. Maeneo makubwa ya hizi reserves kwa lugha ambayo anaitumia sasa hivi ndugu yangu Lukuvi kwa wananchi wa kawaida tunaita mashamba pori. Naomba niwafahamishe kama kuna mtu tajiri wa mashamba pori ni Wizara ya Maliasili na Utalii. Maeneo haya yanaitwa hifadhi lakini ukifika ni nyika hakuna miti zilishabaki nyasi na yamebaki maeneo ambayo yanatumika kukusanya rushwa kwa watu wanaokwenda pale kujitafutia riziki, hayana ulinzi wala hayafanyiwi shughuli yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike? Wenzetu wa Finland maeneo haya wametumia PPP, sekta binafsi mnaiita mnaingia concession, wanalima miti kwenye maeneo hayo, Serikali inapata kipato fulani na wale wawekezaji wanapata. Kwa mfano, sisi mahitaji yetu ya mbao ni zaidi ya cubic meter milioni 40. Sasa hivi uzalishaji wetu ni cubic meter 450,000. Soko la mbao la Kenya, soko la mbao la Djibouti, South Sudan, Ethiopia mpaka Muscat wanasomba mbao na wananunua mbao kutoka Tanzania. Uwepo wetu hapa kijiografia na kuzungukwa na nchi ambazo hazina ardhi ya kutosha, Kenya hawana ardhi ya kutosha, Somalia wana vita na maeneo mengine ni jangwa, kwa hiyo tukitumia ardhi yetu ambayo tayari tunayo, naamini tunaweza kabisa kwa export ya mazao ya misitu na revenue ya kutoka kwenye mazao ya misitu kwa commercial plantation kwa kutumia sekta binafsi kuwa zaidi ya dola za Kimarekani angalau bilioni 20 ambayo ni zaidi ya trilioni 40 ambayo ndiyo bajeti ya Serikali. Tukiwa na mkakati wa namna hiyo kwa miaka 20, 25 kule mbele naamini sekta hii inaweza ikatoa mchango mkubwa sana kwa uchumi wa nchi yetu. Naamini kabisa kwamba tukiyatazama mambo haya kwa upana unaostahili kwa kiwango hicho, tunaweza tukaitoa nchi yetu kutoka hapo ilipo kwenda mbali zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuna eneo ambalo tunazungumzia kuangalia upya mikataba ili iweze kuwa na tija kwenye uchumi na kwa wananchi na hasa mikataba inayohusu kodi. Kwenye sekta ya madini kuna mikataba ambayo ilikwishakuwekwa inayozuia Halmashauri zisitoze ushuru wa huduma na mikataba hiyo imefanya Halmashauri zisiwe zinanufaika pamoja na mabadiliko mazuri sana aliyofanya Mheshimiwa Profesa Muhongo. Kwa mfano, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala inadai zaidi ya shilingi bilioni 14 kutokana na malimbikizo ya ushuru wa huduma ambao imekuwa hailipwi kwa sababu mkataba ulifungwa kwamba ilipwe dola 200,000 wakati proper service levy ya 0.3% ni zaidi ya dola za Kimarekani milioni 1.8 kwa mwaka. Kwa hiyo, mnafungiwa mkataba wa kulipa dola 200,000 wakati sheria inasema mlipwe over and above 1.8 million dollar. Kwa hiyo, naomba mambo tuliyokwisha kuyaanza ya kuzungumza ili kurekebisha…
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali naomba niishukuru Serikali kwa hatua mbalimbali inazochukua kukabiliana na changamoto za upatikanaji wa maji nchini. Kimsingi naunga mkono mipango ya Serikali kupitia bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi naomba kuwasilisha maoni kwenye maeneo yafuatayo:-

Kwanza, scheme za umwagiliaji kutokuwepo Shinyanga; pamoja na ukweli kuwa Shinyanga ni kambi la njaa wakati mvua hunyesha na mabonde yanayofaa kwa umwagiliaji yapo, lakini cha ajabu ni kuwa katika mipango ya Serikali hakuna scheme hata moja katika bajeti. Jedwali Namba Nane, Shinyanga haipo kabisa, naomba maeneo yafuatayo yaingie katika mipango ya Serikali:-

(i) Sheme Bonde la Chela;

(ii) Scheme Bonde la Bumva; na

(iii) Scheme Mabonde ya Kashishi na Kabondo.

Pili, bili za umeme na ruzuku ya uendeshaji KASHWASA; kwa zaidi ya wiki mbili sasa Kahama na Shinyanga hakuna maji kwa sababu KASHWASA inadaiwa na TANESCO na hivyo umeme kukatwa. Naomba utaratibu wa utoaji ruzuku KASHWASA uangaliwe upya ili huduma za maji zisikosekane kwa wananchi wa Kahama na Shinyanga kwa sababu za Kiserikali wakati wateja wanalipa bili zao vema Tatu, mradi wa vijiji 100 vilivyoko pembezoni mwa Bonde la Ihelele - Kahama na Shinyanga ahadi ni ya muda mrefu tangu mwaka 2013 lakini kasi ya utekelezaji ni ndogo. Naomba mwaka huu angalau katika Jimbo la Msalala vijiji vya Mwakuzuka, Kabondo, Matinje, Izuga, Busangi, Nyamigege, Vula, Ntundu, Buchambaga, Mwaningi, Bubungu, Ntobo na Mwankima vipatiwe maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitashukuru kama maeneo haya yatazingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuzungumza. La pili naomba niseme bajeti ni nzuri, naiunga mkono, nishauri tu kama ambavyo Wabunge wengi wamesema kwamba eneo la maji au fedha tulizotenga kwa ajili ya maji bado tatizo ni kubwa ni vizuri eneo hili likatizamwa angalau fedha zikaongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia suala hilo la bajeti, naomba nizungumzie suala la mapato ya Serikali. Kama tunavyojua bajeti unahusu mapato na matumizi na unapozungumzia mapato ya Serikali na hasa kwa Mbunge unayetoka Bulyanhulu huwezi ukaacha kuzungumzia suala la makinikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, kwa hatua ambazo amezichukua kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi tumezungumza. Naomba nilifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba kuna Mbunge mmoja amezungumza hapa kwamba kuna Tume nyingi zimewahi kuundwa na akasema tume hii ya Profesa Osoro na Profesa Mruma ni idadi tu ya nyongeza ya Tume.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimfahamishe Mbunge huyo aliyesema hivyo kwamba pengine hajachukua muda wa kufuatilia naomba nifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba tume ya Bomani ambayo mimi nilikuwa mmoja wapo pamoja na wenzangu kina Dkt. Mwakyembe kazi yetu sisi tuliambiwa tufuatilie/tufanye mapitio ya sera na sheria kuangalia na nchi zingine wanafanyaje ili tutoe mapendekezo kwa Serikali kwa ajili ya kurekebisha maeneo ambayo hatufanyi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya kazi kwetu hatukua tunafanya uchunguzi (investigation) ndiyo maana tume yetu tulikuwa tunafanya kazi kwa kufanya mikutano ya hadhara tunatangaza tupo wapi wananchi wanakuja wanaeleza na hayo tuliyajumuisha kwamba wananchi wa maeneo wanayozunguka migodi wana mawazo haya. Kwenye eneo la usafishaji kwa mfano wa makinikia observation ya Kamati ilikuwa ni kama ifuatavyo naomba nikusomee tulisema hivi; “kukosekana kwa mkatakati wa kisera wa uanziswaji wa viwanda vya uchenjuaji na usafishaji wa madini hapa nchini kumesababisha madini na mchanga wa dhahabu kusafirishwa nje ya nchi kwa ajili ya usafishaji na uchenjuaji, hali hii imesababisha Serikali kushindwa kudhibiti aina na kiasi cha madini kinachozalishwa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia observation hii ya Kamati inaonesha kwamba kuna “smoking gun” inaonyesha kwamba kuna tatizo kwenye hili, ndio maana sasa Mheshimiwa Rais Magufuli sasa akaunda Tume ya kuchunguza kwa hiyo, tofauti ya hizi tume za mwanzo za ushauri na mapitio ya sera, Tume ya Profesa Mruma na Tume ya Profesa Osoro zilikuwa zinachunguza jambo hili mahususi kwamba kuna nini na kitu gani ambacho kinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo jipya amblo halijafanyika, kwa hiyo, Tume ya Osoro na Tume ya Mruma ni tofauti na Tume ya Bomani na kwa mara ya kwanza sasa tunapata tume mahsusi kwa ajili ya kuchunguza, na baada ya hatua hiyo matokeo ya uchunguzi yalipopatikana hatua zimechukuliwa very aggressively, very bold, very fame, very patriotic. Ni kwa approach hii niliwahi kusema hata kwenye kuchangia bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwamba kampuni kama ya Acacia ndipo inapoweza kuja kwenye mazungumzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema kwa wawekezaji hawa ni arrogant, ni fedhuli katika hali ya kawaida si rahisi wakaja kwenye meza ya mazungumzo bila kuwabana na bila kuwa na data za kutosha za kiuchunguzi, ndio maana leo unawaona wanakuja kwa sababu uchunguzi umefanyika na imedhihirisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, na wananchi wa Kakola, wananchi wa Bulyanhulu wanampongeza sana na tayari wameshamuomba Mkuu wa Wilaya awaruhusu wafanye maandamano kama itawezekana kwa ajili ya kupaza sauti zao maana wamepoteza ardhi, wamepoteza wenzao na mambo mengine lakini amepatikana mkombozi ambaye hatua anazochukua zinagusa kabisa mioyo yao na maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hilo naomba nizungumze local issues na hili nimuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini na Mheshimiwa Profesa Kabudi ambaye wanazungumza au wanasimamia suala hili wananchi wa kule ambako makinikia yanatoka wanaona kabisa kwamba na wanaomba issue zao zizingaiwe, zitizamwe na ziwepo katika majadiliano yatakayo fanyika baina ya Serikali na mwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo tunaomba litizamwe pamoja na kuibiwa huku kwenye Serikali Kuu na Halmashauri tumeibiwa, kwa takwimu za Profesa Osoro Halmashauri ya Wilaya ya Kahama na Wilaya Msalala tunadai kati ya shilingi bilioni 795 hadi shilingi trilioni mbili bilioni 283 za service levy kwa takwimu za Profesa Osoro kwa uzalishaji wa Bulyanhulu na Buzwagi kati ya mwaka 1998 hadi 2017. Tunaomba jambo hili halmashauri fedha hizi ziwemo katika majadiliano na Halmashauri tuzipate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili uchunguzi ufanyike kuangalia makampuni mengine ambayo ni related companies ambazo zinafanya biashara kwa sababu zimekuwepo na hii tunaita transfer price bills, makampuni yanayotoa huduma kule hayalipi service levy, kwa hiyo, tunataka kujua yamefanya biashara kiasi gani ili Halmashauri tuweze kutoza service levy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu tunaomba sana katika mikataba na practice za kimataifa, mwekezaji anatakiwa kutumia angalau asilimia moja ya mapato yake kwa ajili ya huduma za kijamii. Kwa kutumia takwimu za Profesa Osoro toka mwaka 1998 hadi 2017, Kahama tunapaswa tuwe tumewekezewa au tumesaidiwa kwenye miradi ya kijamii asilimia moja ya uzalishaji wa Acacia ambayo ni sawa na shilingi trilioni 1.320. Kwa hiyo tunaidai cooperate social responsibility tufanye reconciliation kile walichofanya na trilioni 1.320 ili tuweze kulipwa kinachohitajika kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunaomba lifanyiwe uchunguzi ni kwa kuna madai ya wafanyakazi wanaugua, wako wafanyakazi wengi nilikuwa nikiongea sana na Waziri wa Kazi wafanyakazi wanaopata madhara ya kiafya, kwa hiyo, ufanyike uchunguzi kuhusu afya za wafanyakazi na waliokuwa wafanyakazi na wengine ambao wamekwisha kuathirika walipwe fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuna wananchi 4,600 waliondolewa kwenye lile eneo hawakulipwa fidia yoyote, kwa hiyo, katika majadiliano suala la compensation nalo lizingatiwe na likumbukwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapendekeza kwa kuwa haya yameonekana kwenye makinikia peke yake tunaamini hata kwenye vitofari vya dhahabu nako kuna matatizo. Kwa hiyo, uchunguzi uongezeke tuangalie kwenye vitofali na kwenye migodi mingine, haiwezekani TMAA wakawa wachawi kwenye Bulyanhulu halafu wakifika Geita Gold Mine wakawa watakatifu, practically na kule kuna matatizo uchunguzi ufanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho wote tunajua kwamba mwekezaji huyu amekubali kujenga smelter na tunajua makinikia yanatoka Bulyanhulu na smelter itajengwa Tanzania, niombe Wizara na waratibu wa suala hili basi wafahamu kwamba economically na mazingira yote smelter tunaomba ijengwe pale ambapo makinikia yapo, tunaomba smelter ijengwe Bulyanhulu, naomba mtufahamishe mtuambie inatakiwa ardhi kiasi gani na maandalizi ya namna hiyo yaanze tutenge ardhi, muweze kujenga smelter. Sitaratjii kusikia kwamba smelter inajengwa sehemu nyingine yoyote tofauti na Kahama kwa sababu za mazingira hayo ambayo tunayajua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo naomba niseme napongeza sana bajeti hii namuunga mkono sana Mheshimiwa Waziri na bajeti yake lakini kubwa zaidi wananchi wa Bulankulu, wananchi wa Msalala wanampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hatua anazochukua tunaomba haya maeneo ya uchunguzi yanayohitaji kufanyiwa uchunguzi zaidi yafanyiwe uchunguzi, madai ya wananchi mbalimbali ambayo wananathirika na jambo hili yajumuishwe katika majadiliano baina ya Serikali na mwekezaji ili wakati Serikali inalipwa zile trilioni 108 na sisi Kahama tunalipwa bilioni 795 service levy tunalipwa vile vile trilioni 1.320 kwa ajili ya cooperate social responsibility.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo kwenye hii mada iliyoko mezani. Kwanza naomba tu niungane na Waheshimiwa Wabunge na hasa Wajumbe wa Kamati hizi mbili kwa taarifa walizotoa na kimsingi nakubaliana na mapendekezo yao kwa maana ya maazimio ambayo wameyaweka kwenye ripoti zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo, na mimi naomba ni-register masikitiko yangu kwa jinsi ambavyo mambo yanakwenda kwenye sekta hii. Mwaka 2017 nilifanya ziara kwenye jimbo langu kujionea hali ya mazao kwa wakati ule, nilikumbana na tatizo kubwa la funza. Nilichukua kumbukumbu na niliwasiliana na Wizara kueleza kwamba kuna mdudu ambaye ametokea kipindi kile ambaye anaharibu sana mazao ya wakulima na tukaomba kwamba ni vizuri Serikali ikatoa mwongozo wa dawa gani itumike kukabiliana na mdudu huyu. Hatua hazikuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu 2018 mdudu yule amesambaa mikoa karibu 10 sasa nasikia taarifa, mpaka maeneo ya Kilimanjaro amefika, wakulima wa mahindi karibu wote ambao wamelima hii awamu ya pili, hizi mvua za pili zinazoendelea kwa mfano, katika Mkoa mzima wa Shinyanga, hawatapata mazao yao vizuri. Nilikuwa naomba sana, siyo vizuri kugombana hasa kwa watu mnaoheshimiana kama ambavyo sisi Wabunge tunavyoheshimiana na Mawaziri wetu na Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapopata nafasi, aeleze ni hatua gani ambazo zimechukuliwa kukabiliana na mdudu huyu. Pamoja na kwamba mwaka huu na mwaka 2017 tumeshapoteza mazao, lakini angalau tatizo lisiwe endelevu kutokea tena mwaka unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusu tatizo la pembejeo, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alipokuja na pendekezo hapa la kuanzisha bulk procurement ya mbolea, lilikuwa ni jambo ambalo Wabunge wengi tulilikubali, lakini maelezo aliyoyatoa wakati ule hayajatekelezwa kikamilifu katika level ya implementation. Mheshimiwa Waziri alituahidi kwamba atakuwepo mnunuzi mmoja wa mbolea atakayepata kazi ile, atakayetoa bei ya chini kuliko washindani wote na atakuwa na mawakala kwenye maeneo yote na mawakala wale watatangazwa, watajulikana na bei elekezi zitatolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama atuambie, Wakala wa Mbolea au wa Pembejeo kwa Wilaya ya Kahama ni nani, anauza mbolea kwa kiasi gani kwa kila mfuko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inavyoonekana ilikuwa ni gear kwa ajili ya hoja ile ikubalike, lakini utekelezaji wake umeachiwa njiani. Nilikuwa naomba sana maeneo haya Mheshimiwa Waziri aje atusaidie. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, naomba kuunga mkono mapendekezo ya Kamati zote mbili. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukura sana na mimi kunipa nafasi ili nichangie hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagilaji.

Kwanza naomba nipongeze sana juhudi zinazofanywa na Serikali hii Awamu Tano na kwa kiasi kikubwa kama ambavyo umesema kwamba kazi inayofanyika wa awamu hii inaonekana dhahiri. Yawezekana katika maeneo mengine yanaweza ikawa haijadhihirika sana lakini wanasema unapotapa ni vizuri ukasema ukweli. Miradi ambayo imeanzishwa na inatekelezwa kwenye Jimbo langu la Msalala kwa sasa hivi ni mingi na mikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka mwaka 2014, tulikataa bajeti ya Wizara ya Maji hapa tukitaka fedha zitengwe kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji na hasa vijiji vilivyokuwa kandokando ya bomba kuu la Ziwa Victoria hadi Kahama na Shinyanga. Tuilipitishiwa fedha kwa ajlili ya kuanza kutekelezwa mradi wa Kagongwa Isaka, shilingi bilioni nane, wakati ule Naibu Waziri akiwa Mheshimiwa Amos Makala Waziri wa Maji akiwa Mheshimiwa Profesa Maghembe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka mwaka 2015 mradi ule ulikuwa haujatekelezwa, mwaka 2015 Mheshimiwa Riasi John Pombe Magufuli amechukua nchi, akafika Isaka akasema ndani ya miezi sita mradi huo utakuwa umeanza kutekelezwa. Tumesikia hapa kwamba sasa hivi wakandarasi wako karibu 40 wakitekeleza mradi huu. Naomba pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, lakini nimpongezea pia Mheshimiwa Wazri na Naibu wake. Kwa kiasi kikubwa wanajitahidi sana kusimamia miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisemee mawili tu ya ujumla ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wameyazungumzia; kwanza usimamizi wa miradi hii. Ni kweli ukisikia fedha zilizotengwa karibu katika kila mradi ni hela nyingi sana. Mradi wa Isaka zaidi ya shilingi bilioni ishirini, mradi wa Bulyanhulu bilioni karibia kumi na saba. Miradi yoote hii ukiangalia fedha zinaengwa na utekelezaji wake mara nyingi unakuwa hauwiani. Mimi nishauri sana, Mheshimiwa Waziri umesikia jitahidi sana kuwa na mfumo mzuri wa usimamizi wa utekelezaj wa hii miradi, fedha ni nyingi lakini utekelezaji unakuwa haukidhi viwango.

Mheshimiwa Spika, suala la pili nilitaka kumshauri Mheshimiwa Waziri na hasa Serikali kwa ujumla wake kwamba tukubali hili wazo la kuanzisha mfuko maalum wa maji utakaokuwa na wakala wake unaojitegemea. Tumeona mifumo ya namna hii ambavyo inafanya kazi vizuri kwenye maeneo mengine. Tumeona kwa mfano REA wanafanyakazi vizuri kwa sababu kwa kiasi kikubwa fedha zinatengwa na zinakwenda kwenye eneo maalum ambalo limelengwa kwa ajili hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunaona kwenye barabara TANROADS wanavyofanya kazi vizuri kwa sababu wana Mfuko wa Barabara. Pamoja na changamoto zinazokuwepo za kibajeti kiujumla, lakini angalau miradi inakwenda vizuri. Kwa hiyo, mimi nilikuwa naomba sana, Waheshimiwa wengi wamesema na mimi nirudie ombi hilo kwamba ni vizuri sasa Serikali likakubali hili wazo la kuanzisha wakala maalum na mfuko maalum wa maji na hasa utakaokuwa unalenga vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vyanzo vimepekezwa, kwenye mafuta na maeneo mengine lakini kubwa ni kuwa na wakala maalum unajitegmea ili kutoka kwenye haya makucha ya kumtegemea Dkt. Mpango kila wakati ambaye mwisho wa siku anawapa asilimia 22.

Mheshimiwa Spika, wakiwa na mfuko unaojitegemea hawatapeleka kwa Dkt. Mpango au wakipeleka wanajua kabisa mfuko wa maji zimekusanywa kiasi fulani lazima zitapelekwa bila kusumbuliwa kama inavyotokea sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu la ujumla nilitaka kushauri pia juhudi ziongezwe katika schemes za umwagilaiji, ziwe nyingi zaidi. Tumeona mvua zilivyo nyingi lakini mwisho wa mwaka utajikuta tena kuna maeneo mengine tunalalamika kuna tatizo njaa kwa sababu maji yanatiririka mikoa ya Dodoma, Mikoa ya Shinyanga, hii yenye ukame, yanatiririka lakini hakuna namna ya kuyatunza kwa kilimo cha umwagilaji.

Mheshimiwa Spika, niombe sana Mikoa hii ya Shinyanga na Dodoma iwe na schemes maalum kwa ajili ya kufanya kilimo cha umwagilaji ili tuweze kuondokana na tatizo hili. Kwetu pale Msalala tulikuwa tumeshaanzisha tangu mwaka 2014 ulikuwepo mradi wa scheme za umwagiliaji, Mradi wa Kahanga ulikuwepo sasa hivi kwa Halmashauri ya mji pamoja na mradi wa Chela. Miradi hii ilitengewa fedha hazikutoka zote na haukutekelezwa. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapopata nafasi ukija Kahama tukumbushane ili uweze kutembelea mradi wa umwagilaji scheme ya Chela. Utasikitika kwa sababu umeachwa asilimia 40 ya utekelezaji wake, fedha zimepotea, umwagiliaji haufanyiki na hakuna chochote kilichofanyika na ilikuwa ahadi ya Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda alikuja Chela wakati huo na akasema mradi huo ungefanyika. Kwa hiyo, haya matatu nilitaka niombe sana Wizara izingatie.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwemye miradi ya Msalala, kama ambavyo nimesema miradi ipo mingi, wasiwasi wangu ni utekelezaji wake kwa ukamilifu. Tuna mradi huu isaka kama ambavyo nimegusia, una awamu mbili, awamu ya kwanza inakwenda vizuri, lakini kuna hofu awamu ambayo inahusu usambazaji kwenye vijiji vilivyo kandokando ya bomba kuu, ukachelewa kutekelezwa kwa sababu ya huu mwenendo ambao tunao katika upatikanaji wa fedha na utekelezaji wa mradi wenyewe.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kuomba sana Mheshimiwa Waziri na Wizara yako na Katibu Mkuu yupo hapa na rafiki yangu Mhandisi Karobero - Naibu Katibu Mkuu, wote kwa ujumla sasa muanze utekelezaji wa awamu ya pili kama tulivyokuwa tumekubaliana. Awamu ya kwanza ikifika asilimia 40; awamu ya pili iweze kuanza ili wananchi wa Kata za Mwalugulu, Isakajana waweze kupata maji kwa sababu kwa sasa hivi maji yanapita kwenye kata hizo lakini watapata wananchi wa Isaka Mjini na wananchi wa Kagonga Mjini, lakini Kata ya Isagehe, Mwalugulu, Isakajana hazitapata maji na ziko ndani ya kilometa nane/sita; chini ya kilometa 12. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi mwingine ni huu niliyougusia wa Bulyanhulu kutoka Manghu kwenda Bulyanhulu. Mradi huu nao tulikubaliana utekelezwe kwa ushirikiano baina ya Serikali na mwekezaji wa ACACIA. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, ACACIA mimi nawafahamu, nimefanya nao kazi miaka yote, commitment yao ilikuwa kutoa dola milioni mbili, nadhani mnafahamu; mpaka hivi tunavyozungumza tumesaini mkataba na mkandarasi toka mwezi Desemba, mpaka sasa hivi hata advance haijatoka lakini ACACIA alishatenga dola milioni mbili, zaidi ya bilioni tano ambazo ziko lakini hazijatoka.

Kwa hiyo, nilitaka kuomba tu kwamba muwe macho na huyu mwekezaji, hakikisheni hizi fedha kweli zimetoka, ziko kwenye mfuko ambao Serikali inaweza ikazi-access na ikatumia kulipa wakandarasi, vinginevyo tutapigwa changa la macho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulishaahidiwa mambo mengi kule, mimi nawajua na nimekuwa nikiwalalamikia hapa kila wakati. Kwa hiyo, tutauita mradi wa amoja kati ya ACACIA na Serikali lakini mwisho wa siku utakuwa ni mradi wa Serikali peke yake. Kwa hiyo, nataka kuhimiza hilo, Serikali mlione na mzingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia awamu ya pili ya mradi huu, kama nilivyosema ule wa Isaka nao una sura hii hii, kwamba unapita kwenye vijiji, lakini tulikubaliana phase ya kwanza angalau bomba kuu liweze kufika Ilogi, vijiji vya pembezoni havipati maji. Itakuwa ni tatizo kubwa pale mradi utakapokuwa umefika, bomba kuu lipo, vijiji viko pembezoni havipati. Utekelezaji wa awamu ya pili unaosambaza maji pembezoni mwa hilo bomb kuu na kusogeza mradi huo hadi Lunguya kama tulivyokuwa tumekubaliana nao uweze kuanza kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, hatua za utekelezaji awamu ya pili ya miradi wa Isaka na Bulyanhulu ianze sasa hivi kwa sababu commitment tuliyoiweka kwa wananchi ni kwamba ifikapo mwaka 2020 wananchi wa Kata za Bulyanhulu, Bugarama, Lunguya, Busangi, Kashishi, Isaka, Mwalugulu na Isakajana wawe wamepata maji. Leo ni mwaka 2018 bado mwaka mmoja na nusu au miwili muda huu umefika wa kuja kuulizwa tumefikia wapi. Sipendi ifike wakati huo tuanze kuulizwa maswali ambayo tungeweza kuyaepuka kwa sasa hivi. (Makofi)

Nashukuru sana, kama nilivyosema naunga mkono bajeti, niombe tu Waziri asimamie awamu hizi zitekelezwe kwa ukamilifu. Nashukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru na kimsingi nilikuwa nimeshasimama kwa ajili tu ya kusemea hili la maafa. Kimsingi mimi nimesimama kuunga mkono hilo wazo, lakini nilichotaka kuomba ni kwamba chochote tutakachokifanya kiwe ni kwa Tanzania nzima kwa sababu madhara yako kwa nchi nzima, isiwe kwa Kilwa peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hilo, naomba nami nirudi kwenye mada. Nazipongeza sana Kamati zote mbili, kwa niaba ya Bunge lako zimefanya kazi kubwa sana. Kipekee naomba niipongeze sana Serikali yangu kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi wamesifu, kazi zinazofanyika ni kubwa na nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo wamesema Waheshimiwa Wabunge wengi, nikianza na Sekta ya Umeme, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa rafiki yangu Dkt. Medard Kalemani na Wizara kwa ujumla, wamefanya kazi nzuri na kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, nifafanue tu kidogo kwa sababu katika Jimbo langu la Msalala tulinufaika na REA II ambayo katika Kata 18, Kata 12 tayari zilishaunganishiwa umeme; na hivi sasa kwenye hii REA III utekelezaji wa mradi unaendelea lakini umeanzia upande wa Halmashauri nyingine. Namwomba tu Mheshimiwa Waziri kwamba wananchi wanalifahamu hili, lakini angalau ule mpango wa ujazilizi uende kwa kasi kidogo kwa sababu tayari kuna Kata 12 tuna umeme, lakini hata maeneo hayo ambayo umeme umeshafika kama Busangi, Segese, Lunguya na Kakora, umeme upo lakini bado haujasambazwa vya kutosha.

Mheshimiwa Spika, naomba Meshimiwa Waziri alitazame hili na ninaamini anaweza kwa sababu kama ambavyo wengi tunamwona, amefika kwangu mara mbili, amelizungumzia suala hili na ninaamini kwamba litafanikiwa kwa mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kipekee nitumie muda mwingi zaidi kwenye eneo la madini. Kama ambavyo unafahamu mimi natoka ulipo mgodi wa Bulyanhulu na kwa miaka yote 15 ambayo nimekuwa Mbunge nimekuwa nalalamikia sana namna ambavyo sisi wananchi tuliopo pale ambavyo tumekuwa tukiishi na mgodi wa Bulyanhulu.

Mheshimiwa Spika, na baada ya Mheshimiwa Rais kuwa amechukua hatua hizo alizochukua hizo alizochukua mwaka 2017, nilisimama hapa Bungeni nikampongeza sana, na nilisema kwamba kiukweli kwa sisi tunaoifahamu Acacia ilivyokuwa, ilikuwa haiwezekani kuleta mabadiliko kwenye sekta ya madini bila kuwa na Rais mwenye msimamo na approach ambayo Rais Magufuli ametumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tu nilikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba manung‟uniko kwenye sekta ya madini hayajaanza leo na jitihada za kurekebisha mambo yalivyo kwenye sekta hiyo haijaanzia kwa Mheshimiwa Rais Magufuli. Mwaka 2005 Mheshimiwa Rais Kikwete anaingia madarakani, moja ya vitu alivyovizungumzia na kuvifanyia kazi ni suala la madini. Alianzisha Tume ya Bomani na mimi nilikuwa mjumbe, tukafanya kazi kubwa. Baadaye ikasababisha kupendekezwa na kupitishwa Sheria ya Madini ya mwaka 2010; na tukaanza zoezi la kuwaomba hawa wawekezaji waingie kwenye platform mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lile halikuzaa matunda makubwa kwa sababu ya Acacia. Ikumbukwe kwamba Acacia ndiye mwekezaji mkubwa kwa Tanzania, ana migodi mitatu. Kwa mwaka 2012 dhahabu iliyozalishwa Tanzania wakia milioni 1.3; migodi ya Acacia ilizalisha zaidi ya asilimia 60. Kwa nguvu hiyo waliyokuwa nayo walikuwa ni kikwazo kikubwa sana katika kuleta mabadiliko kwenye sekta hii.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, miongoni mwa mambo yaliyopendekezwa na Tume ya Bomani ilikuwa ni kuhakikisha wananchi waliopo jirani na maeneo ya mgodi wanalipwa fidia stahiki. Wenzetu wa Mgodi wa Geita walifanya hivyo; Vijiji vya Mtakuja, Nyamalimbe na Katoma vikalipwa fidia. Toka mwaka 1996 mpaka leo Mgodi wa Bulyanhulu ulipoanzishwa hakuna kijiji hata kimoja kilicholipwa fidia pamoja na kwamba mgodi upo kwenye eneo la vijiji. Kisa ukiwauliza wanasema tuna MDA the issue is the government, sisi ni wawekezaji; kwa kifupi walikuwa wanagoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukapendekeza, na Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 ikapendekeza mrabaha utoke asilimia tatu hadi asilimia tano na baadaye asilimia sita; migodi mingine ikakubali wao wakawa wamekataa. Tukasema service levy isilipwe kwa lump sum ya dola laki mbili, iwe 0.3 percent migodi ya Geita GGM wakaanza kulipa, Acacia wakakataa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kila kilichokuwa kikifanyika, Acacia walikuwa ni kikwazo. Ilikuwa haiwezekani kufanya mabadiliko kwenye Sekta ya Madini bila kuwa-engage seriously hawa. Na pale jitihada za kuwa-engage kidiplomasia kwa lugha ya kawaida ambayo wengine wanapenda zitumike, zilipofanyika ilishindikana. Ndiyo maana Mheshimiwa Rais baada ya kuja na hii approach ambayo ilisababisha dunia nzima kujua kwamba kweli Maige amekuwa akisema Acacia ni wezi, imekuja kuthibitika kwamba kweli wamekuwa wakitorosha madini.

Mheshimiwa Spika, tusingeyakamata yale makontena ambayo yapo Dar es salaam na kufanya uchunguzi wa kilichomo mle na kuitangazia dunia kitu gani kipo mle, dunia isingejua. Kwa kufanya hivyo kwa kuonesha kwamba kweli Acacia wana matatizo, ilisababisha the whole word ikawa on our side na ndio maana wao wenyewe wakaja mezani na wakawakana Acacia wakaja Barrick wanasema tuzungumze. Wangekuwa hawatendi makosa au wangekuwa hawakutenda makosa wasingekubali na tusingefika hapa tulipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kimsingi nampongeza sana Mheshimiwa Rais, amefanya kazi kubwa sana na Mungu azidi kumsaidia. Akifika; na wote mnajua mliofika Kakola na Bulyanhulu mnajua kilio cha wananchi wale, leo hii ukifika Kakola, Bulyanhulu na Msalala wananchi wana furaha sana hatua iliyofikiwa ni kubwa sana. Naipongeza sana Serikali na nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hiyo hatua ambayo imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais lakini Mheshimiwa Waziri amelisimamia vizuri sana suala hili, suala la wachimbaji wadogowadogo. Baada ya kuwa Serikali imeanza kubana hawa wawekezaji wakubwa mwaka 2015, uzalishaji wa dhahabu ukasimama Mgodi wa Bulyanhulu, tulitegemea uzalishaji wa dhahabu na mapato yanayotokana na dhahabu yashuke; lakini cha ajabu mapato yanayotokana na sekta ya madini yameongezeka kutoka bilioni 130 hadi zaidi ya bilioni 300. Nini kilichofanya matokeo hayo; ni kwa sababu ya kuruhusu wachimbaji wadogowadogo.

Mheshimiwa Spika, leo hii soko dogo la Kakola pale kwangu linauza zaidi ya kilo nne za dhahabu kila siku. Soko la Madini la Kahama linauza zaidi ya kilo 20 za dhahabu kila siku, na hizi zote zinatoka kwa wachimbaji wadogowadogo. Maeneo ambayo wakati wa nyuma yalikuwa yamezuiwa yamewekwa kwenye utafiti wa makampuni makubwa, leo wanafanya wachimbaji wadogo na hizi dhahabu tunapata na maisha yanaendelea. Nawapongeza sana Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, kwa hii dakika moja/mbili zilizobaki nizungumzie maboresho kidogo ambayo yanapaswa yafanyike. Na Mheshimiwa Waziri Biteko naomba unisikilize sana. Kwa kuwa maeneo mengi hayana proper licenses, wachimbaji wanaochimba sasa hivi ni wale wenye vikundi; kumekuwepo matatizo mawili; la kwanza kumekuja mtindo wa wasimamizi kuwa wanachukua asilimia 30 ya mawe yanayochimbwa, hili jambo linaleta mgogoro mkubwa. Hii ada ya usimamizi ili Serikali ipate asilimia saba yake, anapewa mtu asilimia 30 ya ada ya usimamizi, wapi na wapi? Ndiyo maana unakuta mgogoro pale Namba Tisa unajua nilikueleza.

Mheshimiwa Spika, wanakuja watu sasa hivi tunaanza kupambana na mabeberu wa ndani kwa sababu vile vikundi vya wananchi wa pale havipewi nafasi, wanakuja mabeberu wa ndani, na nilishakupa majina, wale watu wanapewa usimamizi. Leo hii Wisolele wanasema wachimbaji wadogo wadogo wa pale hawawezi wakapewa kibali cha kuchimba mpaka yule mtu aliyemtaja ambaye nilisema anahusiana na mtu fulani kwenye kamisheni na yule mwingine na yule mwingine. Ninatunza majina kwa sababu Mheshimiwa Waziri tulishaongea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake sasa hivi kumeanza kutokea manung‟uniko, hebu Mheshimiwa Waziri lirekebishe hili wachimbaji wadogowadogo kupitia vikundi vyao ambao wapo kwenye maeneo wapewe vibali na waendelee kuchimba, hili litatusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Waziri nijaribu tu ku-observe, kwamba hivi sasa Kamisheni ya Madini inachukua asilimia saba ya mawe, lakini pia wanapokwenda ku-process kwenye ile mialo, dhahabu inayopatikana na kwenye elusion wanapopata dhahabu nako inachukuliwa asilimia 7. Ukiangalia kiuhalisia ni kwamba kuna double royalty; tusichukue marabaha kwenye mawe.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi tumeshadhibiti utoroshaji wa dhahabu, tuchukue mrabaha kwenye dhahabu, haya mawe yasimamiwe vizuri, yaende kwenye proper registered sijui kiingereza wanaitaje lakini kwa Kiswahili tunaita mialo, yaende kwenye proper registered mialo, pale dhahabu ikipatikana asilimia saba ichukuliwe.

Mheshimiwa Spika, unajua wachimbaji wadogowadogo waliopo kule wengi wao unakuta wapo kwenye vikundi wanakuwa kikundi cha watu 20, wanapata mifuko 50 wakichukua mifuko 50, mifuko ya Serikali inakuwepo labda mifuko nane. Ikishachukuliwa mifuko nane wanatoa na gharama zingine unajikuta kila mchimbaji anapata mfuko mmoja au robo mfuko, wanatesema sana. Wale wachimbaji kabisa kwa maana ya wale wanaoingia kwenye mashimo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali, hatua hizi ni kubwa na nzuri lakini haya madogomadogo ambayo nimeyazungumzia yaweze kurekebishwa.

Mheshimiwa Spika, la mwisho; tumefanya makubwa na tumefikia hatua kubwa ya kuanzisha hii kampuni ya Twiga. Niombe madai ya wananchi wa Bulyanhulu toka mwaka 1996 kama migogoro mingine ya wafanyakazi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Ezekiel bahati mbaya muda haupo upande wako.

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, sentensi moja tu. Na migogoro ya hawa wafanyakazi waliofukuzwa na wengine wagonjwa, hebu tuimalize. Mheshimiwa Waziri tulishaongea lipo kwenye hatua ya mwisho. Basi kwa hayo, naunga mkono hoja naamini Serikali itaendelea kutenda mema, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema, mimi na sisi sote tuliopo hapa ili tuweze kuwawakilisha wananchi wetu kama ambavyo Katiba inataka tufanye.
Pili, naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuitikia maombi ya Watanzania. Mwaka 2014/2015 Watanzania tulikuwa tunaomba katika imani zetu mbalimbali. Tuliomba kwamba tupate Rais mwenye maamuzi, tuliomba kwamba tupate Rais mwenye vitendo, tuliomba kwamba tupate Rais mwadilifu na tuliomba kwamba tupate Rais ambaye kweli atakuwa ni mtetezi wa wanyonge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi binafsi nimeshiriki katika maombi kwa nyakati tofauti na ushahidi kina mama Jenista Mhagama, tumeshiriki nao tukimuomba Mwenyezi Mungu kwamba atupatie Rais ambaye atakuwa ni mtetezi wa wanyonge. Kinachotokea nchini kwetu dhahiri inaonyesha kwamba Rais John Pombe Magufuli wa Awamu ya Tano ni mwitikio wa maombi ya Watanzania. Ni Rais aliyetoka kwa Mungu na mimi ninaamini mtu yeyote akijaribu kumbeza atakuwa anabeza maamuzi ya Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa kujiamini na kwa uwazi kabisa na kwa dhati ya moyo wangu, kwa sababu yapo mambo mengi ambayo yamekuwa ni hadithi ya miaka mingi leo tunayaona yakitokea.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka miaka yote tulikuwa tukizungumzia kwa mfano sekta ya utalii ambayo mimi nimewahi kuhudumu, kwamba ili uweze kukuza uchumi wa nchi ni lazima uangalie miundombinu na hasa usafiri wa anga. Na ili kukuza utalii tukasema tunahitaji sana Shirika la Ndege la Tanzania liweze kufufuliwa. Kufufua kwa Shirika la Ndege la Tanzania kunamaanisha kwanza, tunatangaza nchi yetu, lakini pili, tunaongeza idadi ya wageni wanaotembelea nchi yetu, na jambo la tatu na muhimu zaidi, ili kunufaika na idadi ya wageni unaowapata ni lazima uangalie wageni hao wanatumia fedha zao kwenye maeneo yapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa tafiti zilizofanyika, asilimia zaidi ya 65 ya fedha anazotumia mtalii anayetoka nje anatumia kwenye usafiri hasa usafiri wa anga, usafiri wa nje na usafiri wa ndani na asilimia karibia 25 anaitumia kwa ajili ya accommodation. Kwa hiyo, ili Taifa liweze kunufaika na idadi kubwa ya watalii inaopata ni lazima tuboreshe na tufufue Shirika letu la Ndege. Kimekuwa kilio cha Watanzania, leo ATCL imefufuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitashangaa kumsikia Mtanzania ambaye anajua maana ya kukuza uchumi, akibeza maamuzi hayo. Tumezungumzia sana kuhusu mawasiliano hasa ya reli, mimi wananchi wangu pale Isaka ilifika mahali wakawa wamekata tamaa, hotuba zote nilizokuwa ninawaeleza walikuwa wanaona kama ninawadanganya. Leo wameshuhudia uwekaji wa jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge. Ni mambo ya kihistoria ambayo yalikuwa hayajawahi kutokea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuitikia maombi yetu Watanzania kutuletea Rais ambaye alihitajika sana kwa wakati huu tulionao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme jambo lingine moja, hata nidhamu Serikalini sasa ipo na hata hapa Bungeni niliwahi kufika wakati fulani kule nyuma kipindi cha Bunge kama hiki, watu ambao walikuwa hawana nia njema na nchi hii walikuwa wanajaa kwenye mahoteli, wanakutana na Wabunge kuweka mashinikizo ili Serikali iweze kufanya mambo ambayo wanayataka. Ilifika mahali Serikali ikawa inaundwa kutoka nje ya matakwa ya Serikali yenyewe. Linawekwa shinikizo mtu fulani afanyiwe hivi kwa sababu tu wameathirika na maamuzi yaliyofanywa na viongozi wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo uhuni huo haupo, Serikali ipo stable na Mawaziri wanafanya kazi kwa kujiamini. Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwa na msimamo na kutumia vyombo vilivyowekwa Kikatiba katika kumpa ushauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Profesa Mbarawa. Kwenye hotuba yake ya mwaka uliopita nilisema kwamba kwa kiasi kikubwa hakunifurahisha, lakini alinieleza kwamba Mheshimiwa Mbunge barabara yako ya kwenda Kahama kwenda Geita hatujaiwekea fedha wakati huu kwa sababu tuna madeni ya wakandarasi wa miradi inayoendelea. Ninakuhakikishia awamu ijayo ambayo ni bajeti hii barabara hiyo itakuwemo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia Hotuba ya Mheshimwia Waziri na nimemsikiliza. Ukiangalia aya ya 257 ya hotuba yake bila kupepesa macho amesema barabara ya Kahama kwenda Geita itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Naompongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa maamuzi hayo, ni Waziri muungwana alichokisema ametenda, ninajua wapo wengine kwa namna moja ama nyingine wanaweza matarajio hayajafikiwa kwa wakati huu. Lakini niwaombe mbona mimi mwaka uliopita niliambiwa nitulie nikatulia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwaombe sote kwa pamoja bajeti hii ni nzuri sana na niwaome katika upigaji kura wote tuunge mkono bajeti hii kwa sababu matarajio ya wananchi na maombi ya kwetu yamekuwemo. Naomba kwa kumalizia, kwa sababu Mheshimiwa Waziri ameonyesha usikivu, nimpongeze sana pia Katibu Mkuu Engeneer Nyamuhanga kwa sababu haya yamefanyika kwa ushauri ambao akimpa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuweka maombi ya nyongeza ambayo ninaamini kwa ushahidi huu tulionao sasa yatatekelezwa. Kuna barabara ambayo ilikwisha kuwekwa kwenye Ilani kwa ajili ya kuanza kujenga ujenzi wa kiwango cha lami, barabara ya kutoka Kahama - Bulige - Mwakitolyo - Salawe hadi Mwanza. Kwenye kitabu hiki inaonyesha kuwa itafanyiwa up grading pamoja na rehabilitation ya kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba sasa angalau kwenye bajeti ijayo, kama tulivyofanya mwaka huu, najua kwamba angalau feasibility study haitaweza kufanyika mwaka huu basi mwaka ujao iweze kufanyika feasibility study. Lakini pia kuna barabara nyingine inayotoka Kahama inaunganisha na Karume makao makuu ya Nyang’hwale kwenda hadi Mwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kwa upande wa Sengerema na Geita, wamekwisha kuanza kuifanyia maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Kipande cha kutoka Kharumwa makao makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale kuja hadi Kahama hakiko kwenye mpango wowote wa Serikali kwa ajili ya kuweka kiwango cha lami. Nimuombe Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla angalau hii barabara na yenyewe ili ikamilike kama ambavyo ipo designed iwe kwa kiwango cha lami kutoka junction ya Nyambula kupita Busangi kupita Nyang’holongo kwenda mpaka Kharumwa hadi Mwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema; Mheshimiwa Waziri alipomaliza hotuba yake mimi nilisimama. Pamoja kwamba mimi ni Mbunge wa kawaida lakini niliunga mkono hotuba tu kabla ya kufika kwenye hoja yenyewe. Naomba nikuhakikishie nakuunga mkono Mheshimiwa Waziri, naunga mkono bajeti hii kwa asilimia 100 na ninaomba nikuhakikishie nitafanya kampeni ili bajeti hii ipite kwa sababu maombi yangu na maombi ya Waheshimiwa Wabunge tulio wengi umeyazingatia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi naomba niseme naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa na nzuri inayofanyika katika kufanya mabadiliko kwenye maeneo mbalimbali ambayo tumekuwa tukiyalalamikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwa baadhi ya Wabunge ambao nimesikia hapa wakijaribu kutuelekeza namna ya kusema; nawaomba wasifanye hivyo, kwa sababu Wabunge hapa tuko wengi, nchi yetu ni kubwa na mazingira yanatofautiana sana. Kwa hiyo, mawazo ambayo nitayatoa kutokana na mazingira yangu ya Msalala ni tofauti sana na mawazo ya Mbunge mwingine. Kazi ya Serikali ku-coordinate na kuweza kuchukua hatua za kurekebisha pale ambapo pana marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba mambo yaliyofanyika ni makubwa. Changamoto zilizoko kwenye kilimo ni kubwa sana, lakini hatua zinazofanyika zinaonekana. Tumelalamikia sana kwa mfano suala la tozo mbalimbali, kwamba linaumiza wakulima. Hatua zimechukuliwa, tumeona, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi kumekuwa na tatizo kubwa sana la uratibu na usambazaji wa mbolea. Mpango na utaratibu uliokuwepo kwa miaka yote ulikuwa unasababisha matatizo makubwa ya upotevu wa fedha za Serikali, lakini kubwa zaidi hata usambazaji wenyewe ulikuwa unafika wakati mbolea inasambazwa kwa kuchelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa hatua iliyochukuliwa ya sasa ya kufanya uratibu na usimamizi wa ununuzi wa mbolea kwa kutumia huu mtindo wa bulk procurement.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuunge mkono wazo hili, naamini litatusaidia. Tumekuwa na matatizo, hii ni hatua mojawapo ya kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ushauri wangu kwenye hili eneo la mbolea ni kwamba ni lazima sasa kwa sababu mbolea itaagizwa na sekta binafsi ni lazima Serikali iweke utaratibu mzuri wa kuthibiti bei; kama ilivyo kwenye mafuta kwamba wanaagiza na wanaelekezwa bei ya kuuzia kwenye maeneo mbalimbali watakayosambaza, pia bei elekezi ya mbolea itakayosambazwa iweze kutolewa na hao wasambazaji na mawakala wao kwenye hayo maeneo, waweze kutangazwa na wajulikane kwamba Wakala wa Mbolea kwa eneo kwa mfano kwangu Kahama ajulikane ni fulani na bei yake itakuwa ni hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nishauri hivyo kwenye eneo la mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika utangulizi, mimi natoka Mkoa wa Shinyanga. Mkoa huu kwa miaka yote tumekuwa tukilalamikia tatizo la njaa. Naomba nifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba hata sasa hivi Mkoa wa Shinyanga hali ya chakula hairidhishi. Tumetoka kwenye kipindi chenye changamoto za mvua za vuli mwezi, Novemba, Disemba, zimenyesha kweli. Kufika mwezi Januari, mvua zilikata kabisa na sehemu kubwa waliokuwa wamelima mahindi, hasa Wilaya ya Kahama, mahindi yote yalinyauka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa mvua za masika zimeanza kunyesha tena mwezi wa Pili, wakulima wakajaribu tena kulima kwa mara nyingine, lakini cha ajabu kukatokea funza! Siyo viwavijeshi, lakini ni aina fulani ya funza wa ajabu sana ambao wameharibu mazao yote. Mheshimiwa Waziri tuliongea kwamba moja ya tatizo kubwa tulilolipata kama wananchi na wakulima ni kutokupata mwongozo wowote kutoka kwa Maafisa Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walikuwa wanahangaika kukabiliana na hawa funza bila kujua watumie dawa gani? Wapo waliokuwa wakishauriwa watumie sabuni na kuchanganya na majivu, haikusaidia; wapo walioelekezwa kutumia dawa za mifugo, haikusaidia; na mwisho mazao hayajapatikana. Kwa hiyo, naomba katika msimu ujao wa kilimo ni muhimu Serikali kuwa imeshajua tatizo la hawa wadudu ni nini? Au hao wadudu ni wa aina gani? Dawa gani itumike?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoiomba Serikali hapa, siyo lazima itununulie dawa, ielekeze tu kwamba wadudu hawa wanauawa kwa dawa hii, wakulima tumieni dawa hiyo. Itawasaidia sana wakulima. Watu wa Shinyanga ni wakulima wazuri, wala hawahitaji kusukumwa kwenda shambani. Kwa mazingira tuliyonayo kwa sasa, kabla ya kufika msimu ujao wa kilimo, tutakuwa na tatizo la njaa. Nilikuwa naiomba sana Serikali, kumekuwepo na utaratibu wa Serikali kusaidia mbolea kwa miaka ya nyuma na kusaidia kuwezesha maeneo mengine ambayo mvua zinanyesha, wazalishe kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtizamo ni kwamba huko wanakozalisha, mikoa ile ya G5 Iringa, Morogoro, Rukwa na kadhalika, wazalishe kwa wingi. Halafu baada ya kuwa wamezalisha chakula kile kiweze kuuzwa kwa bei nafuu kwenye mikoa ambayo ina shida kama Shinyanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali kwa hiki kipindi isaidie kuratibu zoezi hili. Wafanyabiashara ukiwaelekeza tu bila kuwasaidia namna yoyote ya kuwapa incentive, bado hawawezi wakafanya biashara na hawawezi wakapunguza tatizo la bei. Kwa hiyo, naomba sana Serikali kwa hiki kipindi kabla ya msimu ujao wa mvua, ifahamu kwamba Mkoa wa Shinyanga tuna tatizo la uhaba wa chakula na isaidie kuratibu upatikanaji wa chakula cha bei nafuu kabla ya kufika msimu ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu ujao utakapofika, naimba sana Serikali isaidie jitihahada za Serikali ya Mkoa wa Shinyanga kuanzisha kilimo cha umwagiliaji. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge Azza kwamba mwaka 2010/2011 Serikali ya Mkoa wa Shinyanga iliandaa mpango kabambe wa kupambana na njaa katika mkoa na iliweka mkoa katika kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanda mojawapo iliyobuniwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji, ni Halmashauri ya Wilaya Shinyanga Vijijini kwa maana ya Jimbo la Solwa pamoja na Jimbo la Msalala ambalo lina bonde zuri sana linalotoka maeneo ya Mwakitolyo kuungana kule kutoka mkondo wa Ziwa Victoria hadi kuja kwenye Kata za Mwanase, Kashishi, Bulige, Isaka pamoja na Isakajana kwa jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maeneo yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji na taarifa zilishafika Wizarani. Naomba sana, jitihada hizi zilizoanzishwa na mkoa ziungwe mkono na Serikali ili badala ya kuomba chakula kila wakati, badala ya kuomba Serikali iingilie kati kupunguza bei ya chakula katika eneo hili, wananchi hawa waweze kulima na mvua zinanyesha, pamoja na kwamba zinanyesha kwa muda mfupi, maji yanapatikana, basi waweze kulima kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu tulipendekeza kuanzisha Soko la Kimataifa la mchele kwenye eneo la Bulige na mradi ukawa umekwishaanza kwa maana ya kuanza kujenga soko. Kwa bahati mbaya uendelezaji wa mradi huo mwaka 2013/2014 ukawa umesuasua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara isikume mradi huu utekelezwe ili kama mkoa tulivyopanga na Halmashauri na Jimbo kwamba mpunga uzalishwe kwa wingi kwenye eneo hili la Solo na Msalala na soko kubwa la mchele liweze kuwepo pale Bulige; na kwa kufanya hivyo umasikini utapungua na wananchi wataweza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia kwa dakika chache zilizobaki, nataka kuishauri Serikali kwa upande wa uvuvi, ielekeze nguvu katika ufugaji wa samaki. Uvuvi wa samaki kutoka kwenye mabwawa na maziwa ambayo tayari yapo, hauna tija sana. Tujifunze kutoka nchi kama Vietnam ambayo zaidi ya asilimia 80 ya samaki wanaouzwa kwenye soko ni wale wanaofugwa kwenye vidimbwi vidogo vidogo. Jambo hili linawezekana na linaweza kikaongeza sana tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa migogoro ya wakulima na wafugaji, naomba sana Serikali iongeze juhudi katika kusaidia wafugaji kupata malisho. Ukisikiliza chanzo cha migogoro, ni malisho versus maeneo ya kulima. Sehemu kubwa ya maeneo makubwa ambayo yamekuwa malisho miaka ya nyuma kwa mfano Mkoa wa Shinyanga ambao unalima na kufuga, maeneo mengi ambayo yamekuwa ni ya mifugo, sasa wanalima. Kwa hiyo, wafugaji wanajikuta hawana maeneo ya kufugia, wanaendelea kuhama kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na mjadala kuhusu suala hili kwamba yatapatikana maeneo ya kuwasaidia wafugaji wawe na maeneo yao watakayoyamiliki na kufuga bila kuhama. Naomba Serikali iharakishe kukamilisha zoezi hili ili maeneo ya wafugaji yajulikane, maeneo ya wakulima yawepo ili migogoro iweze kwisha. Siyo jambo zuri kukaa tunalalamikia jambo hilo miaka nenda, rudi na mwisho wa siku tunashuhudia mauaji ya wakulima au wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla, mpango wa Serikali ni mzuri, pamoja na kwamba kuna maeneo ambayo naiomba Serikali iongeze nguvu. Naiunga mkono bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana rafiki yangu Mheshimiwa Dkt. Tizeba na rafiki yangu, mtani wangu, Mheshimiwa Olenasha, ongezeni juhudi, sisi Wabunge tunaelewa mnachokifanya, tunajua mnafanya kazi kubwa na tutaendelea kuwaunga mkono. Tusaidieni katika hayo ambayo nimeyasema na Wabunge wenzangu wameyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi niseme machache katika mada hii inayoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia naomba niseme nakubaliana na pendekezo au hoja iliyoko mezani naiunga mkono, nina mambo machache tu ya kushauri lakini kabla ya hayo ya kushauri naomba nianze kwanza kutoa pongezi sana kwa hatua ambazo zinachukuliwa na Mheshimiwa Rais za kuongeza mapato ya Serikali na kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze kipekee Mheshimiwa Rais kwa hatua ambazo amekuwa akizichukua kwenye suala zima la madini. Nadhani unafahamu na Bunge lako linafahamu kwamba mimi ndiye Mbunge wa Bulyanhulu. Mbunge ambae nimekuwa nikiishi na mgodi wa Bulyanhulu kwa miaka yote, nimekuwa nikizungumzia sana kuhusu Serikali kutokupata stahiki yake pamoja na wananchi, Wabunge wengi tumekuwa tukiungana kwenye hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishtuka sana juzi Jumatatu, pamoja na hatua nzuri sana iliyochukuliwa na Mheshimiwa Rais, zikatokea baadhi ya sauti hapa Bungeni zikitutisha kwamba eti tunaweza tukapata shida. Nawaomba sana Watanzania wenzangu, mimi kama Mbunge wa kule,
naomba muamini kwamba nchi inaibiwa. Tunaweza tukabishana kwenye kiwango cha wizi lakini suala la kwamba tunaibiwa halina ubishi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya 2008 na 2009 niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge, wananchi wa kawaida kabisa vijijini walianza kuwa wanayavamia yale malori yanayosafirisha mchanga na kuiba ule mchanga, kwenye viroba vile vya mfuko wa saruji vya kilo 50 walikuwa wanaweza wakachenjua kwa kiteknolojia ya kienyeji na kupata dhahabu na mfuko mmoja walikuwa wanapata siyo chini ya shilingi milioni 50. Kufuatia hatua hiyo, wawekezaji walianza kusafirisha yale malori usiku kwa ulinzi mkali kuonesha kwamba kuna mali nyingi inayosafirishwa. Nilishtuka sana kusikia Watanzania wenzetu wakitia mashaka juhudi hizo za Rais, niwaombe sana na nikuombe Mwenyekiti na Bunge lako Tukufu watu wa namna hii inabidi pengine tuanze kujiuliza sana kuhusu Utanzania wao na uadilifu wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani hata kidogo kwamba katika nchi ambayo ina uwekezaji mkubwa na rasilimali nyingi za namna hiyo ukifika leo Kakola, tena wao wenyewe wamekuwa wachochezi wa kwanza, wakifika pale wanasema hivi hapa kuna Mbunge? hakuna maji, hakuna hiki, hakuna hiki kwa sababu wanasema wanapata hasara. Wanapata hasara kwa sababu dhahabu iliyoko kwenye container la tani 20 wana-report kwamba kuna kilo nne wakati kuna kilo 28. Kwa hiyo kwa record za performance ya kilo nne lazima utasababisha hasara, lakini ukiweka kwa hesabu ya kilo 28 kwa container lile lazima una faida kubwa. Kwa kufanya hivyo maana yake wangeweza kuwa wanalipa corporate tax, wangeweza kufanya mambo mengi ambayo tunapaswa kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana tuungane kwenye hili jambo ni vita kama ambavyo Mheshimiwa Rais amesema na wananchi wa Msalala nilikuwa Kakola juzi nimeongea na wananchi wangu, wanamuunga mkono sana Rais na tunaomba Bunge lako limuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tu kwamba katika mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Bomani yako mengi yaliyosemwa na machache yametekelezwa kwenye ripoti hiyo, nitaomba tu nikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba pengine ni vizuri report hiyo ikarejewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, moja ya vitu vilivyopendekezwa na Tume ya Bomani ni kwamba, katika dunia na nchi zote tulizozunguka mimi nikiwa Mjumbe, ilionekana kwamba hakuna sehemu ambayo wana utaratibu wa ku-share manufaa yanayotoka kwenye mgodi kama tunavyofanya Tanzania, kwenye nchi zingine wana revenue sharing plan, kwamba eneo ambalo kuna mgodi wanapata percent fulani kutokana na kodi na tozo mbalimbali ambazo zinatokea au zinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba baadhi ya mapendekezo ambayo hayajatekelezwa na Serikali yarejewe na yatekelezwe, hata hili la kujenga smelter limo tulikwenda mpaka Sumitomo mimi mwenyewe nilikwenda na tukashauri kwamba Serikali ijenge smelter……

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru na naunga mkono hoja, nitazungumza tena kesho kwenye Wizara ya Nishati na Madini.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano, hususan Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ya ujenzi wa miundombinu katika maeneo mbalimbali nchini. Naomba kusema, naunga mkono bajeti hii kama sehemu ya kuunga mkono juhudi hizi za Mheshimiwa Rais na Serikali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo, naomba yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, ujenzi wa barabara ya Kahama - Geita uanze. Kwa miaka mitatu mfululizo tumekuwa tunatenga bajeti lakini fedha hazitolewi na ujenzi hauanzi. Hii ni bajeti ya mwisho kabla ya uchaguzi mwakani, hatuna cha kuwaambia wananchi. Mheshimiwa Rais pamoja na Ilani kuahidi, pia aliahidi wakati wa kampeni mwaka 2015 na alipofanya ziara Shinyanga mwaka 2017, bado ujenzi hauanzi. Naomba sana, tuanze ujenzi hata kidogo ili tupate cha kusema mwakani.

Mheshimiwa Spika, pili, usanifu wa barabara za Kahama – Bulige – Solwe – Mwanangwa, Kahama - Nyang’hwale - Busisi, Kahama – Kaliua - Mpanda na Kagongwa – Itobo – Bukene – Tabora. Ukamilishwe haraka ili ujenzi uanze kama Ilani yetu ya CCM ya mwaka 2015/2020 ilivyoahidi.

Mheshimiwa Spika, tatu, ujenzi wa reli kwa SGR kati ya Dodoma – Tabora – Isaka - Mwanza utaanza lini?

Mheshimiwa Spika, nne, ujenzi wa reli ya kisasa Isaka - Kigali umefikia hatua gani?

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naomba nianze kwanza kwa kupongeza sana hatua nzuri au kazi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi na Taifa linafahamu tuna bahati sana kipindi hiki kupata Rais mwenye maamuzi, kupata Rais ambaye analitumikia Taifa kwa dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi ambayo inafanyika sasa hivi ni miradi ambayo imekuwa ni ndoto ya Watanzania ya muda mrefu na ninaamini kabisa baada ya kukamilika kwa miradi hii hakika tutakuwa Tanzania ambayo itakuwa na uchumi wa kati, uchumi ambao utakuwa unaendeshwa kwa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana sasa Waheshimiwa Mawaziri ambao hasa ndio wanamsaidia Mheshimiwa Waziri Mkuu na Rais, mtusaidie pamoja na sisi wenyewe katika kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais, katika kuhakikisha tunafikia malengo ambayo tunajiwekea. Nitazungumzia mambo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni suala la upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo. Katika ahadi tulizozitoa kwenye sekta ya afya pamoja na elimu, tulisema kwamba tutajenga vituo vya afya kila kata pamoja na zahanati kila kijiji. Baada tu ya kuwa tumewaahidi hivyo kwa mfano wananchi Jimbo langu la Msalala wameitikia vizuri sana na kama ambavyo wengi mlisikia hata hapa juzi Naibu Waziri wa TAMISEMI alitambua kazi iliyofanyika kule kwamba hivi tunavyozungumza tuna maboma zaidi ya 50 ya zahanati na vituo vya afya; mengi yana miaka miwili na zaidi, wananchi wameshafanya kazi lakini fedha za ukamilishaji haziletwi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu Wizara zote ziko yako, wasaidie Watanzania hasa ambao ni wananchi wa kawaida waliojitikia na kuchangia nguvu zao kuinua maboma haya ili fedha za ukamilishaji ziweze kutolewa kwa wakati. Imefika wakati kwa mfano kuna sehemu ambapo wananchi tunawahimiza waanzishe miradi mingine wanasita kuchangia kwa sababu tayari kuna miradi ambayo wameshaianzisha imekamilika kwa kukamilika maboma, lakini fedha za ukamilishaji haziletwi kwa hiyo, wanaona kwamba yanaenda kubomoka au kuharibika na nguvu zao kupotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe sana Serikali itoe fedha za ukamilishaji wa maboma ya zahanati na vyumba vya madarasa pale ambapo majengo hayo yameshakamilika na tayari tulishaandika andiko la kuleta taarifa rasmi Serikalini kuhusu suala hili kwa maana ya Msalala peke yake basi nilikuwa naomba Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nilitaka kutoa ushauri kwa Mawaziri tupunguze sana kugongana na wananchi pasipo sababu za msingi. Nitatoa mfano wa suala mifugo na uvuvi. Operation iliyofanyika juzi ya uvuvi kudhibiti makokoro ni jambo jema, lakini nilitaka kumshauri sana Mheshimiwa Waziri Mpina bahati nzuri yuko hapa kwamba sasa tujaribu kuwasaidia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufahamu kwamba vyazo vya asili vya samaki haviwezi vikatosheleza Watanzania milioni 50 tulionao hivi sasa. Duniani kote nchi zinazosafirisha samaki wengi au mazao ya samaki kwa wingi zimeweka nguvu kubwa kwenye fish farming. Eneo hili la uvuvi wa ufugaji wa samaki hatujaliwekea maanani sana.

Mheshimiwa Mweyekiti, Nchi kama Vietnam ambayo ni nchi ya nne kwa usafirishaji wa mazao ya samaki duniani, asilimia 70 ya samaki wanaosafirishwa nje ni wale wanaofugwa sio wale wanaovuliwa kwenye bahari kuu au kwenye maziwa na mito. Ninaamini ziwa victoria ambalo limekuwepo miaka yote limekuwa likihudumia wananchi karibia milioni nanewa miaka ya nyuma, leo hii watanzania wanaozunguka eneo hili wamefika zaidi ya milioni 20. Hauwezi ukatarajia hata ukifanya vipi mahitaji ya samaki au mahitaji ya mazao ya samaki yataendelea kuwa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kwa mfano kwenye suala la kuku miaka nyuma tulipokuwa tukitegemea kuku kawaida wa kienyeji wa kutoka Singida ilikuwa ni tatizo. Lakini baada ya kuanzisha ufugaji wa kuku wa kisasa hawa broilers, leo pressure ya mahitaji ya kuku wa kienyeji si kubwa kama ambavyo ingeweza kuwa kama tusingeweka nguvu katika ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine ni kwenye suala la maliasili, ukiangalia tungeendelea kupambana na wananchi, tungeendelea kupambana na wananchi wanaovuna kwenye misitu ya asili tusingeweza kama tusingeweka nguvu katika…

(Hapa palitokea hitilafu ya umeme ndani ya ukumbi wa Bunge na kusababisha moshi kutaanda ukumbini)

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana, naomba niwape Waheshimiwa pole Waheshimiwa Wabunge kwa tafrani hii lakini naamini sasa hali ipo shwari tuendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nazungumzia suala la kuwasaidia Watanzania waweze kuzalisha rasilimali ambazo zinatokana na kufanya kazi. Nilikuwa nasema kwa upande wa uvuvi, pengine itakuwa ni jambo la busara sana Wizara ya Mifugo na Uvuvi kusaidia wananchi waingize nguvu au wafanye kazi ya kufanya fish farming. Kwa kufanya hivyo tutaweza kupunguza migogoro ya wananchi badala ya kuelekeza nguvu katika kudhibiti wananchi kuwadhibiti wasivue samaki kwenye maziwa ya asili na mito vyovyote vile production au uzalishaji samaki kwenye maziwa ya asili utakuwa umepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nilikuwa ninaiomba sana Serikali kwa upande wa mifugo vilevile tumeshatambua mifugo yetu, tumeshaitia alama sasa kinachotakiwa ni kuwasaidia wakulima au wafugaji kwa maana hiyo waweze kuwa na masoko ya mifugo yao. Wafugaji tumepambana nao tumewatoa kwenye maeneo ya hifadhi. Wanauliza swali la msingi kwamba sawa tumetoka hifadhini tuende wapi? Kuna mkulima mfugaji mmoja kuna wakati alikuwa ananiuliza kwamba hivi hawa ng’ombe mnataka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nishukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri na kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais. Kazi kubwa ambazo zinafanyika kwa sasa katika sekta hii ya ujenzi Watanzania wote tunaona. Hakuna ubishi kwamba katika kipindi cha miaka 10 cha Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tutakuwa na Tanzania tofauti sana na Tanzania ambayo tumekuwa nayo kwa zaidi ya miaka 50 ya uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi, nina mambo machache yafuatayo ambayo kimsingi ni maswali tu ambayo nataka Mheshimiwa Waziri au Naibu wake wakati wa kuja kutoa majumuisho anisaidie. Nafahamu na kwenye vitabu nimeona lakini wananchi wanauliza na mimi pia nauliza, mwaka jana kwenye bajeti ya 2017/2018 tulipitisha shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Kahama – Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mazungumzo ambayo nimekuwa nikiyafanya na Wizara hii toka muda huo ni kwamba baada ya bajeti kuwa imepitishwa kilichokuwa kinafuata ni utaratibu wa kumpata mkandarasi. Leo ni mwezi wa nne, mimi na wananchi hatuna taarifa zozote kuhusu utaratibu wa kumpata mkandarasi wa kujenga barabara ya Kahama - Bulyanhulu - Geita umefikia hatua gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye bajeti ya mwaka huu tumeongeza tena fedha zingine, tumetenga shilingi bilioni 13 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa barabara hiyo, lakini kwa sababu wananchi hawaoni chochote kinachofanyika on the ground inakuwa siyo rahisi kuamini kwamba kweli barabara hii itakwenda kujengwa. Namwomba Mheshimiwa Waziri atuambie ni nini hasa kilichofikiwa katika ujenzi, kupitisha bajeti hata mwaka jana tulipitisha lakini haitoshi wananchi wanataka kuona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tulikusudia kufanya Kahama iwe makao makuu ya kiuchumi kwa kanda hiyo. Ili kufikia azma hiyo tulisema ni muhimu sana kufungua barabara zinazounganisha Kahama au Shinyanga na maeneo mengine. Kuna barabara kama tatu ambazo zinaunga Kahama na Mkoa wa Mwanza kupitia Jimbo la Msalala ambazo sijaziona zimefikia hatua gani angalau kuanza kufanyiwa upembuzi yakinifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kutoka Kahama - Nywang’wale - Busisi - Sengerema - Mwanza. Nimeona upande wa Mwanza kuna upembuzi yakinifu umeanza kwa ajili ya kutengeneza daraja la Busisi. lakini barabara inayounganisha sasa daraja la Busisi hadi Kahama haijawekwa katika mpango wa kufanyiwa upembuzi yakinifu. Napenda sana jambo hili nalo nisikie limefikia hatua gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kutoka Kahama – Mhongolo - Burige - Solwa – Mwanangwa – Mwanza. Barabara hii ilikuwa ijengwe kwa MCC lakini kwa bahati mbaya fedha zile zilipoondoka ikawa imeingizwa kwenye mipango ya Serikali lakini sioni kama imewekwa katika mpango wa kufanyiwa upembuzi yakinifu. Nataka barabara hizi mbili niweze kuambiwa kitu gani kinaendelea au ni hatua gani imefanyika hadi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilimsikia Rais wa Rwanda Mheshimiwa Paul Kagame akiwaelekeza viongozi wa Wizara ya Tanzania na Rwanda waanze kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga reli kutoka Isaka - Kigali. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri sijasikia lolote kwamba hatua gani imefikiwa sasa kwanza katika kufanya feasibility study na detail design ya reli hii lakini pia hata kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo ya Mheshimiwa Rais niliyasikia vizuri kabisa alisema ifikapo mwaka 2020 angalau hatua fulani ya ujenzi iwe imeanza. Wananchi wa Msalala hasa Isaka na wananchi wa Tanzania kwa ujumla wanapenda kujua hatua gani imefikiwa katika utekelezaji wa agizo hilo la Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ambalo nataka kumalizia ni suala la mawasiliano. Nashukuru Serikali imefanya kazi kubwa sana kupitia wawekezaji wa private sector kuweka minara mbalimbali kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Tatizo tulilonalo ni kwamba maeneo ambayo yamejengwa minara hii wenye minara hawalipi ushuru kwenye halmashauri (service levy) na vilevile hawalipi tozo yoyote ya ardhi kwenye kijiji na hata kwa wananchi ambao ardhi yao imechukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limekuwa ni jambo ambalo wamekuwa wakiliulizia na mara kadhaa tumekuwa tukiongea na Naibu Waziri, Mheshimiwa Atashasta Nditiye kuhusu suala hili, lakini kwa sababu tumekuwa tukiongea binafsi, wakati mwingine tunaongea tukiwa nje ya ukumbi huu ambao ni rasmi, napenda sana angalau leo awatangazie Watanzania kwamba ni utaratibu gani hasa ambao unapaswa kutumika kwa wananchi ili waweze kupata appropriate share ya service levy inayotoka kwenye makampuni ya simu yaliyoweka minara yao vijijini lakini vilevile…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kuniruhusu nami nichangie hotuba hii ya Bajeti ya Mapendekezo ya Serikali kuhusu Mapato na Matumizi yake kwa mwaka huu wa 2018/2019. Kabla ya kuanza kuchangia, nami nina utangulizi kidogo. Kwa muda mrefu sana tumekuwa tunapata lawama upande huu. Wenzetu upande wa barabara ya pili kule, wanaongea na kutusema kila tunapomsifu Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli, kwa mambo mazuri anayoyafanya kwamba wamefanya nchi siyo yeye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani kote viongozi wote wa nchi na viongozi wa Taasisi wanapata sifa zinazofanya na Taasisi zao kwa niaba ya Taasisi hizo. Tumekuwa na Viongozi kama Mheshimiwa Baba wa Taifa, Mheshimiwa Kwame Nkhuruma, Mheshimiwa Mao wa Uchina na wengine wote wamekuwa wanapata sifa za nchi zao za matendo yao kutokana na yale wanayoifanyia nchi. Pia kumekuwa na sifa mbaya, viongozi wanapata sifa mbaya ya matendo yao, kama vile sisi tulivyovamiwa na Iddi Amin. Yeye hakuchukua hata bunduki, waliotuvamia ni Askari wake, lakini lawama akapata yeye. Kwa hiyo, wenzetu upande wa pili wa barabara hii ya kuingilia Bungeni watuache tuendelee kumsifia Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa matendo yake, kwa sababu ndiyo sifa zake zilizomvaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya utangulizi huo, naomba niwashukuru sana na niwapongeze Mawaziri hawa wawili, Mdogo wangu Mheshimiwa Dkt. Mpango na Mdogo wangu Mheshimiwa Dkt. Kijaji kwa kazi kubwa waliyoifanya kuandaa mpango huu wa Bajeti ya mwaka huu wa 2018/2019. Hawa ni Wachumi, wameonesha kwamba wamesomea kazi hii ya uchumi na ndiyo maana wanaitwa Madaktari wa Uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bajeti yako hii, yako mambo mengi kwa manufaa ya wananchi. Hii ni bajeti ya wananchi kwa mara ya kwanza. Serikali ya Awamu ya Tano imeleta Bajeti ambayo sisi Sekta Binafsi tunaiunga mkono; watu wote Viwandani, wanaiunga mkono. Tangu tumeanza kuleta Bajeti hapa Bungeni, tangu nimeingia Bungeni, hakuna Waziri yeyote aliyeleta Mpango wa kusamehe madeni yanayotokana na riba za madeni ya wanaodaiwa na VAT. Hawa wameleta mfano mzuri sana, kwamba sisi, wale ambao tunadaiwa; mimi pia nadaiwa na VAT, naomba ku-declare interest. Nimefurahi sana na sio mimi tu na wafanyabiashara wote, Mheshimiwa Dkt. Mpango, tutalipa madeni hayo kwa kipindi cha miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, bajeti hii imekuja na mapendekezo ya kusamehe ile kilichokuwa kinaitwa zamani kodi ya makampuni ya asilimia 30 na kwenda asilimia 20 kwa baadhi ya makampuni hasa yanayoanzishwa. Pia tumeona kwenye ngozi; na muhimu kabisa tumeona hata taulo za akinamama zimefikiriwa na ilikuwa adha kubwa sana na bei kubwa kwa watu kupata taulo hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninayo machache ya kusemea kama changamoto. Jambo la kwanza ni elimu. Elimu tumeona hapa Mzaramo, rafiki yangu Waziri wa TAMISEMI, ameongelea kwamba wanafunzi waliochaguliwa kwenda sekondari ni asilimia 75,000, lakini bahati mbaya sana wanaopata nafasi, wanabakia wanafunzi wengine 25,000 hawana pa kwenda. Kwa hiyo, njia pekee aliyopendekeza, tujenge madarasa ili tuweze ku-accommodate wanafunzi hawa kwa mwezi wa Nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mie nakuja na pendekezo lingine na naomba lifanyiwe kazi, linaweza likasaidia. Kwa nini tusiingie PPP na shule za watu binafsi ambazo zina miundombinu tayari, lakini tutoe hela ile ile ambayo ni unit cost ya kila mwanafunzi kwa mwaka huu waende kwenye shule zile wakati tunaandaa shule zetu, ziwe tayari kwa ajili ya intake ya mwaka kesho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, PPP inawezekana tunaiongelea ipo kwenye sera yetu; tuitumie kwa mara ya kwanza kwenye elimu, tupeleke wanafunzi hao kwa kuwalipia cost ile ile. Bahati mbaya au nzuri nimefanya research. Ziko shule nyingine za binafsi, cost unit ya mwanafunzi mmoja ni rahisi kuliko cost unit ya wanafunzi wanaolipiwa katika Shule za Sekondari za Serikali au za Upili. Napendekeza basi, Serikali ifikirie PPP na shule binafsi ambazo zitafanyiwa uchunguzi kwamba zinafaa, zinatoa mafunzo sawasawa na za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la pili ambalo pia ni muhimu kuliongolea, nalo ni Elimu ya Ufundi. Nimekuwa nasimama hapa mara kwa mara kwa maana mimi ni zao la Shule za Ufundi, lakini bahati mbaya Serikali inaongolea Sera ya Viwanda, lakini mafundi sadifu, nina maana technicians wa kuendesha viwanda hivyo hawapo, kwa sababu Shule za Ufundi hazitoshi na Vyuo vya Ufundi kipo kimoja tu cha DIT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka mingi imepita, Serikali sasa ione umuhimu wa kuandaa chuo kingine ili kuzalisha mafundi sadifu (technicians) wengi badala ya kukazania VETA ambao wanatoa Artisans, ni kiwango cha chini cha Elimu ya Ufundi. Mafundi watakaoendesha mitambo hii viwandani wanatakiwa wawe na level ya FTC (Full Technical Certificate) au mafundi sadifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu atakapokuja ku-wind-up hii bajeti atuelezee mpango wa kuanzisha shule za ufundi; na ningependekeza shule za ufundi za Kata ili kwenye Kata kuanzishwe chimbuko la mafundi watakaoendesha ufundi wa viwanda vidogo vidogo huko kwenye kata na majimboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la Kiswahili. Kiswahili chimbuko lake ni hapa Tanzania, lakini hakuna sheria yoyote inayosema Kiswahili ni Lugha ya Taifa wala hakuna GN yoyote inayosema Kiswahili ni Lugha ya Taifa. Wenzetu Kenya wameitia ndani ya Katiba ya Kenya, kwamba Kiswahili ni Lugha ya Taifa. Sisi tulikuwa tunaandika hapa Katiba, ile Katiba inayopendekezwa, tuliweka suala hilomle; lakini wakati huu wa ombwe la Katiba Mpya, kwa nini Serikali isije hata na GN tu ili watu waongee Kiswahili badala ya kuongea lugha ambayo haieleweki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa Kiswahili imekuwa kitendawili mashuleni. Watoto wanasoma Shule za Msingi, mpaka darasa la saba Kiswahili. Wakifika Shule ya Upili, wanaanza kufundishwa Kiingereza, hawaelewi masomo, hawaelewi lugha. Nchi zote ambazo zimeendelea; Ufaransa, Uingereza, Marekani, Ufilipino na China wote wanafundisha kwa lugha ya kwao ambayo inayoeleweka. Hivi mwanafunzi akifundishwa Kiswahili, Serikali inaona tatizo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Elimu inasema lugha ya kufundishia Shule za Upili na Shule za Utatu, ni Kiingereza, lakini huu ni Ukoloni. Nchi zote zote zilizojikomboa katika elimu zinafundisha kwa lugha zao. Naomba sana

Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind hili ili suala la mambo yanayohusu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, aongelee Kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala lingine ambalo linaleta gharama kubwa sana katika Bajeti ya Mambo ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Suala la nyumba za Mabalozi wetu; tumekuwa tunapanga nyumba kwa gharama; na asilimia 75 ya gharama zote za Wizara hii ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ni pango za Balozi zetu; Ofisi na nyumba za wafanyakazi. Kwa nini tusiendeleze mpango uliokuwepo wa kujenga majengo ya Mabalozi wetu na nyumba za Makazi? Hata kama tutachukua miaka 10, lakini tutaweza kujenga nyumba hizo ili ziweze kuondoa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye mada iliyoko Mezani. Kwanza naomba nizipongeze sana Kamati zote tatu, wamefanya kazi nzuri sana na kimsingi nakubaliana sana na mapendekezo ambayo wameyaweka. Kwa upande mwingine pia naomba niishukuru sana Serikali, nayo kwa upande wake imefanya kazi kubwa, imetimiza wajibu. Kwa mfano, katika Sekta ya Maendeleo ya Huduma za Jamii na Elimu, yako mambo mengi mazuri ambayo yemefanyika.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwa mfano kwa upande wa Afya jinsi ambavyo Serikali imetoa fedha nyingi kwa ajili ya kujenga Vituo vya Afya kwenye kila Kituo cha Afya ambacho kimependekezwa kwenye Halmashauri, vile vile kuna ujenzi wa Hospitali za Wilaya na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, kwa ujumla nakubaliana na mapendekezo yalitolewa. Naomba tu niongezee kidogo kwenye maeneo ambayo nadhani ni muhimu Kamati hizi zingeweza kuyatazama na kuyawekea mkazo. Nilidhani ikiwezekana nimwombe sana Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii anisaidie katika ku-wind up, kuboresha azimio mojawapo linalohusu upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa sana kama ambavyo nimesema awali, lakini bado kuna maeneo ambayo tunahitaji kuongeza juhudi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa afya na elimu kwa mfano, tumefanya kazi kubwa ya kuhamasisha wananchi waweze kujenga shule; na hapa nitazungumzia hasa Jimbo langu la Msalala kama mfano mmojawapo.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2015 wakati tunafanya kampeni kwa kuzingatia Ilani yetu ya CCM, tuliwaambia wananchi kwamba tutajenga Zahanati kila kijiji na tutajenga Kituo cha Afya kila Kata na vilevile tutajenga shule kwenye maeneo yote ambayo hayakuwa na shule. Tuliwaambia wananchi kwamba mambo haya hatutayafanya sisi kama Serika peke yake na wao wananchi watashiriki; na tuliwaeleza kwamba wanapaswa kuinua maboma na Serikali itawashika mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wameitikia sana. Nilimsikia rafiki yangu Mheshimiwa Mwijage muda fulani anazungumza kwamba sisi kama Wabunge tende tukawahamasishe wananchi wetu kupiga propaganda ili waweze kuanzisha miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naomba nilifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba kazi hiyo nimeshaianza. Hivi tunavyozungumza, tuna maboma 131 kwenye Jimbo la Msalala ambayo wananchi wameshaweka nguvu zao pale, mengine yana miaka mitatu, mengine yana mwaka mmoja na mengine yana miaka mingi kidogo. Tuna maboma zaidi ya 62 ya vyumba vya madarasa. Leo hii tunawahamasisha wananchi sasa waanze kuyajenga wenyewe hadi kuyakamilisha wakati walishakayakamilisha imebaki Serikali kuleta fedha za ukamilishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna maboma 40 ya Zahanati na katika mpango ule tulishawahamasisha wananchi wakanza kujenga Vituo vya Afya kwenye maeneo matatu. Kwa hiyo, kuna majengo makubwa matatu ambayo yanatosha OPD pamoja na vyumba vingine ikiwemo theater kwenye Kata tatu. Kwa hiyo, kwa ujumla tuna maboma ambayo thamani yake iliyobaki inayotakiwa kuyakamilisha ni shilingi bilioni 4,268.

Mheshimiwa Spika, wananchi wameshaweka nguvu zao pale na thamani ya fedha au nguvu ambazo wananchi wameweka pale ni zaidi ya shilingi bilioni 1,623. Kuna hatari kwamba maboma haya sasa yanaeleekea kuanza kubomoka na Serikali haijaleta fedha za ukamilishaji wakati matarajio ya wananchi yalikuwa kwamba wakishakuwa wamemaliza maboma haya, basi Serikali italeta fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii kama ilivyowasilisha Kamati kwenye lile azimio linalohusu kupeleka fedha, basi angalau kama unaona siyo lazima sana kwenye maeneo mengine, basi angalau lile azimio tuliboreshe tuseme kwamba Serikali ipeleke fedha za ukamilishaji wa maboma Jimbo la Msalala…

MHE. SELEMANI J. ZEDI: Na Bukene.

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Na Bukene kama unaona kwingine haipendezi sana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba hili suala la kupeleka fedha za miradi lifanyiwe haraka na liwe sehemu ya maazimio ambayo tungependa kuyaweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizungumzie kwa upande wa elimu na tatizo la ajira. Katika maeneo ambayo tuna matatizo makubwa sana ni suala zima la ajira. Alisema Mheshimiwa Nkamia asubuhi na Waheshimiwa Wabunge wengine, suala la ajira kwa sasa ni janga. Tusipochukua hatua, ninaamini kabisa kwamba linaweza likaleta madhara makubwa kwenye jamii yetu na hata utangamano na ustahimilivu na usalama wa nchi.

Mheshimiwa Spika, ninavyoona tatizo liko katika mfumo wa elimu yetu. Tuna wahitimu wengi ambao wana- graduate kwa sasa hivi, zaidi ya graduates 600,000 kwenda juu, kuanzia level ya Form VI wale wanaokosa nafasi kuendelea na masomo hadi Vyuo Vikuu; wote hawa wanahitaji ajira kwenye sekta iliyo rasmi. Kwa mfumo huu tunaokwenda nao, naamini kabisa hatuwezi kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, tujaribu kujiuliza na nilitaka niwape changamoto Mawaziri wangu wawili hawa; Mheshimiwa Jenista Mhagama na hata Mheshimiwa Waziri wa Elimu, hivi katika intervention za Serikali zinazofanywa, hizi za kusaidia kukuza ajira, jiulize tu, tunaposema asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwenda kwa akina mama, vijana na walemavu, hivi kuna watu wangapi wenye elimu kuanzia Form VI wanaotumia fursa hiyo? Ukipiga hesabu ni kama hawapo. Wanaokwenda kwenye hizo fursa ni Darasa la Saba kwenda chini.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo elimu yote aliyoipata kuanzia Form VI kwenda juu hawaitumii kwenda kujishughulisha kujiajiri, wanawaachia wenzao wa chini zaidi na wao wanasubiri ajira za Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumetoa vitambulisho kwa wafanyabiashara, Mheshimiwa Rais ametoa karibia vitambulisho 100,000 sasa, hivi katika hao wafanyabiashara kuna wangapi ambao wamemaliza Form VI, ukiangalia utakuta ni hakuna. Kwa hiyo, hawa wote kuanzia Form VI kwenda vyuo wote wanasubiri ajira zilizo rasmi.

Mheshimiwa Spika, tuimarishe elimu ya ufundi (polytechnic colleges) ambayo mtu akimaliza pale, tena ikiwezekana hata mkopo tumpatie atoke na cherehani yake, aende ajiajiri, aanze kufanya kazi. Hii ya kumaliza wanagombea boom kule ambalo ndiyo mikopo ya Elimu ya Juu, halafu akimaliza anakaa anaanza kuomba ajira ambazo hazipo, ni tatizo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie mfumo wa elimu ili iweze kuwasaidia vijana wetu waweze kwenda kwenye ajira moja kwa moja badala ya kuwaandaa kuajiriwa kwenye nafasi za white collar jobs ambazo hazitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kujua kwamba muda unaelekea kwisha naomba nimalizei kusema naipongeza sana Serikali na Kamati zote tatu.

Mheshimiwa Spika, nimalizie sentensi kabla sijafunga kabisa, kuhusu suala la TARURA. Ni kweli, sasa hivi utengenezaji wa barabara za vijijini umepungua kuliko ilivyokuwa ukisimamiwa na Halmashauri. Kuna tatizo. Mojawapo ni fedha zinazopelekwa TARURA hazitoshi. Pia hili suala la ushirikishwaji; Madiwani ambao ndio wanaosimamia Halmashauri, wengi wao hawashiriki wala hawajui mipango ipi ambayo imewekwa na TARURA kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, nilidhani eneo hili ni vizuri likarekebishwa; mpango wa kuwaongezea fedha TARURA ufanyike na namna ya kuwashirikisha Madiwani ifanyike ili tuweze kufanikisha lengo la kuwa na TARURA na kuboresha barabara za vijjini.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja zote tatu. Nashukuru sana kwa nafasi uliyonipatia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami naomba nianze kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa juhudi kubwa ambazo zinafanyika katika kukabiliana na tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamezungumza kwamba tatizo la maji kwa sasa lilivyo ni tatizo kubwa sana ambalo naiomba sana Serikali yangu ilitazame kwa mtazamo tofauti. Ni janga ambalo kwa kweli karibia kila mahali kuna kilio kikubwa na jitihada zisipofanyika tukaendelea na mwendo huu tulionao, naamini kila wakati tutaendelea kupokea malalamiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinadharia Jimbo la Msalala kama miradi yote ambayo imepangwa na Serikali kutekelezwa na kama ikitekelezwa katika muda tuliopanga wa kufikia 2020, Jimbo letu litakuwa limebakiza Kata mbili tu ambazo hazina maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali hasa kuanzia Awamu hii ya Tano lakini pia hata Awamu ya Nne kuna baadhi ya miradi mikubwa ilianza kutekelezwa. Kwa kutaja tu baadhi ya miradi, ukurasa ule wa 31 Mheshimiwa Waziri amezungumzia mradi wa maji wa Ziwa Victoria ambao kwa sasa uko kwenye awamu ya pili ya utekelezaji unaogusa vijiji 100 na Jimbo la Msalala lina vijiji vyake kadhaa ambao unaendelea kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi mwingine mkubwa sana wa zaidi ya shilingi bilioni 15 unaotekelezwa kwa ubia kati ya mgodi wa Bulyanhulu (Acacia) pamoja na Serikali yetu. Unatoa maji Mhangu hadi Kijiji cha Ilogi kwenye Kata ya Bugarama. Kuna mradi mwingine mkubwa tu na wenyewe wenye zaidi ya shilingi bilioni 24 ambao unapeleka maji kwenye Mji wa Kagongwa na Isaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii yote ikitekelezwa; na yote ina sura ya awamu. Kwa mfano, mradi wa Isaka na Kagongwa una awamu mbili, mradi wa Mangu, Ilogi na wenyewe una awamu mbili; na miradi hii ikitekelezwa kwa ukamilifu, itaweza kutatua tatizo la maji tulilonalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ifanye juhudi za kutafuta ufumbuzi. Bahati nzuri wazo la kutafuta ufumbuzi au jibu la tatizo tulilonalo limeshatolewa na Waheshimiwa Wabunge hapa. Ukiangalia miradi yote inashindwa kukamilika mapema kwa sababu ya upatikanaji wa fedha ama fedha zinapopatikana kidogo zinakuwa ni zile ambazo ni za mfuko wa maji peke yake, zile za Bajeti Kuu na za wafadhili hazipatikani kwa wakati. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameshapendekeza hapa, nami niungane nao na niseme tu kwa sababu ni jambo ambalo tulishaliamua hapa, ni vizuri sana Serikali ikakubaliana na ombi letu la kwamba angalau tuongeze tozo kwenye mafuta ili tuweze kutatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii niliyoitaja kinadharia ukiisikiliza ni mizuri sana, lakini miradi karibu yote utekelezaji wake uko kwenye viwango tofauti tofauti hakuna ambao uko zaidi ya asilimia 80 na hapo ndiyo tatizo kubwa linapoanzia. Nikianza kwa mfano na ule Mradi wa Vijiji 100; mradi huu tuliuibua hapa Bungeni mwaka 2014, Waziri wa Maji akiwa Profesa Maghembe, tukasema vijiji 100 vilivyoko pembezoni mwa bomba kuu la kutoka Ziwa Victoria hadi Shinyanga vipatiwe maji, Jimbo la Msalala lilikuwa na vijiji 16 katika orodha ya vijiji 100. Mpaka tunavyozungumza hivi sasa vijiji ambavyo vimepatiwa maji ni vijiji vitano tu, kwa hiyo bado vijiji tisa toka mwaka 2014 havijapata maji, hili ni tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ule mradi wa pili niliousema wa kutoa maji Mangu hadi Ilogi kupitia Wilaya ya Nyang’hwale pamoja na Wilaya ya Msalala, naishukuru sana Serikali na hasa Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na Katibu Mkuu wote wawili Katibu Mkuu mwenyewe Profesa Mkumbo na Engineer Kalobelo wameusukuma sana mradi huu hadi kufika hatua hii ya kuanza kutekelezwa. Tuliubuni namgodi wa Acacia mwaka 2012 na toka 2012 hadi mwaka 2014/2015, hakuna utekelezaji uliofanyika, lakini 2016, baada ya Serikali hii kuingia madarakani ikatoa fedha na mradi umeanza kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa uko asilimia chini ya 50 na lengo lilikuwa kufika Desemba, 2018 bomba Kuu la kutoka Mangu hadi Ilogi liwe limewekwa, hivi sasa halijakamilika. Awamu ya pili ambayo ni kusambaza maji kwenye vijiji vilivyo jirani na yenyewe haijaanza. Naiomba sana Serikali ikubali hili ombi la kuongeza fedha kwenye Mfuko wa Maji ili fedha hizo ziweze kutekeleza awamu ya pili ya kupeleka maji kwenye vijiji ambavyo vipo pembezoni mwa hilo bomba kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Kagongwana Isaka na wenyewe tulisema uwe na awamu mbili, awamu ya kwanza ni ile ya kupeleka bomba kuu na kusambaza maji pale Kagongwa na Isaka penyewe, lakini kuna kata tatu ambazo ziko pembezoni ndani ya kilomita 12 zinapitiwa na bomba hilo;Kata ya Mwalugulu,Kata ya Mwakatapamoja na Kata ya Isaka na Kata ya Jana. Vijiji hivi tunaenda kutengeneza matatizo, wanaona maji yanapita kwenda kwa wenzao wa Isaka wao hawapati maji. Tulisema hii ni awamu ya kwanza, vumilieni hadi kufika 2020 wananchi hawa watakuwa wameanza kuona na wenyewe wakitekelezewa mradi huu. Naiomba Serikali yangu wakubali hili ombi ili awamu ya pili ya kupeleka maji katika vijiji vilivyoko pembezoni mwa hilo bomba kuu uweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulibahatika pia kupata ule mradi wa mkopo wa Benki ya Dunia vijiji 10 kila Wilaya. Halmashauri ya Msalala tuna Kijiji kimoja cha Segese kinadai shilingi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri sana.

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, kwa hiyo naomba tu Kijiji cha Segese kinadai milioni 30 ya kufunga pampu, milioni 700 zimewekwa pale, lakini mradi haufanyi kazi. Tunaomba Serikali isaidie ombi hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nanashukuru sana kwa nafasi.(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza naomba niipongeze sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa sana inayofanyika ya ujenzi wa miundombinu mingi mbalimbali nchini na pengine tu kabla sijaenda mbali zaidi, nijaribu kugusia kidogo hii hoja iliyotolewa na mchangiaji mmoja aliyezungumzia kuhusu suala la mchango wa Sekta ya Ujenzi kwenye uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti unaonyesha kwamba katika miradi yote ya ujenzi, asilimia isiyozidi 30 ndiyo huwa mchango wa wakati wa mradi, asilimia 70 huwa inapatikana pale mradi unakuwa umekamilika na kuanza kutumika. Jana tulimsikia mzee wangu Mheshimiwa Ndassa hapa alizungumzia kwamba Mji wa Ngudu umedumaa kwa sababu hauna barabara. Ukienda sehemu zote ambazo barabara zimejengwa, hali ya maisha na shughuli za kiuchumi zinakwenda kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, tunavyozungumza kujenga reli ya kiwango cha standard gauge tunategemea reli hii ikikamilika ndiyo itakayoleta manufaa na itakayoonyesha sasa uchumi kukua kwa kasi zaidi kuliko wakati wa utekelezaji wa mradi wenyewe. Faida zinazokuwepo wakati wa ujenzi ni kidogo sana kwa wastani hazizidi asilimia 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu pamoja na kwamba Mheshimiwa Zitto namuheshimu sana lakini ukweli huu anaufahamu ni vizuri tukaliona hilo kwamba investment zinazofanyika leo zina multiply effect kubwa kwa baadaye hasa baada ya sekta tarajiwa kama kilimo na viwanda. Huwezi ukajenga kiwanda leo Kigoma cha cement ambayo huwezi ukaisafirisha kuipeleka kwenye soko Dar es salaam; ukishaweka reli ndiyo utawezesha kiwanda kujengwa kule. Leo hii muulize Dangote anavyohangaika kufikisha cement yake kwenye maeneo ambayo hayana miundombinu ya barabara. Kwa hiyo, miundombinu inachochea uchumi baada ya kuwa imekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ufafanuzi huo na pongezi hizo kwa Serikali, niendelee kuipongeza sana Serikali yangu kwa miradi hii mikubwa ambayo pia inafanyika katika Mkoa wetu wa Shinyanga. Kwa muda mrefu sana nimekuwa nikiomba barabara ya kutoka Kahama kwenda Geita ijengwe kwa kiwango cha lami, ninashukuru sana nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri aya ile ya 28, amesema taratibu za kupata wakandarasi ndizo zinaendelea na kwa bajeti hii ile aya ya 248 ametenga bilioni 5 kwa ajili ya kuanza ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Mheshimiwa, bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri Kwandikwa yupo na anafahamu barabara hii umuhimu wake kwamba mchakato wa kupata wakandarasi ambao sasa tunakwenda mwaka wa tatu toka 2016, 2017 na 2018 ukamilike na barabara ianze kujengwa. Ni barabara ya muhimu sana kiuchumi, inaunganisha migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi; ni barabara yenye sifa katika zile barabara za kipaumbele kwa sababu inaunganisha Mkoa wa Shinyanga na Mkoa wa Geita. Vilevile ni barabara ambayo ipo kwenye ahadi zetu za kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais mwaka 2017 amefika, ameongea na wananchi wa Segese akawaahidi wananchi wa Bukoli kwamba barabara hii itaanza kujengwa kwenye kipindi hiki na hii ndiyo bajeti ya mwisho ya utekelezaji tunayofanya, bajeti ijayo tutakuja kuipitisha na kwenda kwenye uchaguzi. Ni muhimu sana hizi bilioni 5 tulizozisema na mchakato wa kupata wakandarasi ambao umeanza miaka mitatu sasa ukamilike ili ujenzi uweze kuanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara nyingine ya kutoka Kahama kwenda Nyang’wale hadi Busisi. Barabara hii haijaguswa kabisa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, tuliahidiwa kwenye bajeti iliyopita kwamba ingeanza kufanyiwa upembuzi yakinifu, sasa hivi hata kutajwa haijatajwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata ile barabara ya kutoka Kahama – Solwa – Managwa ambayo pia inaunganisha Mkoa wa Shinyanga na Mkoa wa Mwanza, ilikuwemo kwenye upembuzi yakinifu na ilishakamilika lakini kwenye orodha ya barabara ambazo zimetajwa kwamba zimekamilika kufanyiwa upembuzi zinatafutiwa fedha ili zianze kujengwa, haijatajwa. Nilikuwa naomba sana rekodi zikae sawa, muda wote tuwe tunataja tumefika hatua gani ili kesho na keshokutwa tusijetukarudi tena kuanza kuzungumza kwamba tunaomba ifanyiwe hatua fulani wakati ilishakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe la mwisho, Mheshimiwa Waziri Mpango yupo hapa, nimeona kwenye taarifa ya Waziri kuna ujenzi wa vituo Dakawa na Muhalala; mkandarasi amesimama kwa sababu ya suala la VAT. Nilikuwa naomba suala la VAT ambalo linahusu kuwezesha miradi ya ujenzi kukamilika kwa wakati, mzungumze mlimalize; Mheshimiwa Rais aliagiza akiwa Mwanza wakati ule wa uzinduzi wa ujenzi wa vivuko kule, ninaomba mmalize mkandarasi arudi site, kuna hasara tunapata kwa kutokumaliza mazungumzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimegongewa kengele ya pili, nisingependa kuchukua zaidi muda. Nakushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru sana na mimi kwa kunipa nafasi nichangie mada iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nianze kwa kuipongeza sana Serikali kwa hatua zinazofanyika katika kuboresha sekta ya kilimo. Zimekuwepo kero nyingi kwa miaka ya nyuma lakini hivi sasa unaona kabisa kwamba hatua zinazochukuliwa zinatatua kero hizo. Kama tunakumbuka kwa wale ambao tumekuwa kwenye Bunge hili muda mrefu, shughuli kwa mfano ya bei na usambazaji wa pembejeo za kilimo limekuwa ni tatizo la muda mrefu, lakini utasikia kwa sasa na hata miaka ya baadaye, hatua ambazo zimechukuliwa za ununuzi kwa mfano wa mbolea kwa pamoja unafanya vizuri; na hii ni hatua nzuri sana ambayo kwa kweli naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipongeze vilevile Serikali kwa zao la pamba; uzalishaji unaongezeka sana, tunategemea mwaka huu kuvunja rekodi ya zaidi ya miaka mitano nyuma. Hizi ni jiihada za Serikali yetu. Mimi nampongeza sana Mheshimiwa Rais, Waziri na Naibu Mawaziri wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi hii kubwa inayofanyika wote tunaamini kwamba inatakiwa ilenge katika kuweka uhakika wa chakula katika nchi kwa ujumla wake, pia inatakiwa kuwa ni chachu katika dhana nzima ya Tanzania ya viwanda. Mimi mchango wangu upo kwenye haya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, food security kwa Tanzania bado kwenye baadhi ya maeneo tunapata changamoto. Kwa huu mwaka wa kilimo ambao tunaenda nao, kuna baadhi ya maeneo ambayo hayajapata chakula vizuri kwa sababu ya mabadiliko ya tabia nchi na hali ya hewa kusababisha mvua kutokunyesha vizuri; lakini kuna maeneo ambayo yamepata chakula. Nini solution ya suala hili? Kwa ujumla tumekuwa tukishauri kwamba ni vizuri tukajikita kwenye scheme za umwagiliaji ili kutunza maji yanayopatikana kwa muda mrefu. Suala hili kwa Mkoa wetu wa Shinyanga tumekuwa tukilizaungumza kwa muda, tukiamini kwamba si vizuri Mkoa kila wakati tukisema kwamba tuna matatizo ya njaa basi tunaomba chakula cha msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2013, tulipendekeza katika RCC kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu na Halmashauri ya Shinyanga Vijijini kwa maana ya Jimbo la Solwa na Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, maeneo yake zaidi ya asilimia 80 yanafaa kwa kilimo cha mpunga. Kwa hiyo mkoa ubuni mpango wa kufanya kilimo cha umwagiliaji kwenye maeneo hayo. Zimekuwepo jitihada katika mkoa lakini inaonekana kama vile kuna mawasiliano hafifu baina ya Serikali Kuu, kwa maana ya Wizara na Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Msalala kwa mfano miaka miwili iliyopita tulipendekeza scheme zaidi ya sita. Tulipendekeza kuwepo scheme kwenye Bonde la Kashishi, kuna eneo linaitwa Kashishi kule, ni kubwa tu ambalo likifanyiwa kilimo cha umwagiliaji tunaweza kupata mazao vizuri. Kuna Bonde la Kabondo, Bonde la Buva, Bonde la Chela kuna scheme ilianza mwaka 2008, haikufanya vizuri; na kuna Bonde la Mwalugulu. Kwa bahati mbaya maeneo yote haya ambayo yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji jitihada ambazo zimekuwa zikifanyika kwenye ngazi za halmashauri, hazioneshi kuungwa mkono na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana rafiki yangu, mhasibu mwenzangu, Mheshimiwa Waziri hebu fika Msalala uyaone haya maeneo, uone jitihada ambazo tunafanya katika halmashauri ili uone namna ya kusukuma jitihada hizi ili tuwe na uhakika wa chakula. Tunaamini kabisa jitihada hizi za Wilaya na Mkoa zikiungwa mkono, tutakuwa na uhakika wa chakula. Tunataka maeneo haya ndiyo yawe ghala la mpunga kwa mkoa mzima na tuweze kuzalisha na kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, vilevile kama nilivyosema, kwa upande wa kuunganisha na biashara, kwenye zao la pamba viwanda vinavyoendana na zao hilo bado havijasukumwa sana. Nilitaka kuiomba Serikali kwa maana ya Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Viwanda hebu jaribuni kukaa pamoja ili kuangalia namna ya kuboresha zao la pamba kutoka zao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Malizia Mheshimiwa

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: …hadi linapoweza kutengeneza nguo pamoja na mafuta.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, jitihada zinazofanyika na Serikali ni kubwa na zinaonekana, naiunga mkono bajeti hii. Nimuombe sana tu Mheshimiwa Waziri aje aone jitihada zetu na tuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, napongeza juhudi za Serikali kurekebisha sekta ya madini. Naunga mkono juhudi hizo na mipango ya Serikali kupitia bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali irekebishe na kusaidia wachimbaji kwenye maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, urasimu na mazingira ya rushwa katika utoaji wa leseni za uchimbaji; wachimbaji wadogo wa Msalala kupitia vikundi vyao vya KAGOMCO (Kasi Mpya Gold Mining Cooperative Society) na BMS (Bushimangila, Masabi na Segese Coperative Society) waliomba leseni maeneo ya Mwazimba na Bushimangila. Mheshimiwa Waziri Biteko alikuja Msalala na kuwahakikishia kuwa watapata leseni.

Mheshimiwa Spika, akiwa Bushamangila aliagiza hivyo, cha ajabu baada ya muda mfupi Afisa Madini Mkazi wa Kahama alihamishwa, afisa madini aliyeletwa alitoa leseni kwa mtu mwingine siku moja tu baada ya kufika Kahama, kinyume kabisa na maagizo ya Waziri; hiyo siyo rushwa? Naomba afisa huyo aliyetoa leseni Bushimangila kwa kampuni tofauti na BMS katika mazingira hayo ya rushwa achukuliwe hatua na leseni zitolewe kwa BMS.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa KAGOMCO waliomba leseni Mwagimba tangi 2008 na leseni yao kuingia kwenye mgogoro, naomba mno wapewe leseni yao kama Waziri, Mheshimiwa Biteko alivyoagiza.

Mheshimiwa Spika, kusiadia wachimbaji wadogo kupata exploration data za maeneo wanayofanyia kazi ili kupunguza hasara kwani maeneo mengi yalishafanyiwa exploration na GST na Sekta Binafsi na data hizo Serikali inazo au inaweza kuzipata.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Msalala tunadai Acacia ushuru wa huduma miaka toka 2000 hadi 2014. Jumla ya madai ni dola 8,500, sawa na shilingi 16 bn. Naomba Wizara ya Madini kwa kushirikiana na TAMISEMI isaidie halmashauri yetu ilipwe haki yake.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi bahati mbaya ukunitaja kabla kidogo nijipange. Naomba kwanza niipongeze sana Serikali na hasa Mheshimiwa Rais kwa mabadiliko makubwa, marekebisho makubwa sana yaliyofanyika kwenye sekta hii. Kama mnavyofahamu Waheshimiwa wenzangu mimi natoka mgodi wa Bulyanghulu; nimekuwa na matatizo na kero nyingi ambazo nimekuwa nikizilalamikia hapa lakini kwa kweli awamu hii tumeona kazi kubwa nampongeza sana Mheshimiwa Rais. Nimpongeze sana pia Mheshimiwa Waziri na Nibu pamoja nawatendaji wote wa Wizara pia mnafanya kazi kubwa kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais, pia kusimamia mifumo mipya ya sheria za madini ambayo inanufaisha sana wananchi hasa wachimbaji wadogo wadogo.

Mheshimiwa Spika, nina mambo kama mawili tu ambayo nilitaka kuyazungumzia; kwanza kwa wachimbaji wakubwa. Kama nilivyosema mgodi wa Bulyanghulu una changamoto zake kwa sasa hivi tunafahamu kwamba walishasimamisha uzalishaji na wanaendelea na mazungumzo na Serikali kuhusu migogoro yao ya kule nyuma.

Sisi kama wananchi wa pale tumekuwa tukisema tuna matatizo yetu ambayo tumekuwa nayo kwa muda mrefu; la kwanza ambalo nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri utusaidie; tumekuwa tukidai service levy mapunjo kabla hawajaanza kulipa zero point three percent, walikuwa wanalipa dola 200,000 jumla yake ni kama dola milioni 8.6 ambazo ni takriban shilingi bilioni 16. Tulishaomba kupitia Wizara ya TAMISEMI kwa sababu ni suala liko chini ya halamashauri kwamba Waziri Jafo pamoja na Wizara ya Madini mtusaidie kumbana huyu mwekezaji ili haki yetu tuweze kulipwa. Nilikuwa naomba suala hilo lilwe mezani kwako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka vilevile nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, tulishamweleza kuhusu matatizo ya migogo ya wananchi ambayo imekuwepo pale; kubwa zaidi ni fidia mgodi wa Bulyanghulu ulipoanzishwa mwaka 1996 wananchi waliokuwepo pale ni kaya 4,600, waliolipwa ni kaya 34 tu, na hili suala nimekuwa nikilieleza na Wizara inalifahamu. Tunaomba tuendelee kulifuatilia, suala la fidia kwa wananchi wa Bulyanghulu bado halijawa settled.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ni wachimbaji wadogo wadogo, tuna matatizo ya maeneo kule kwetu tulikuwa tulishaunda vikundi kuna kikundi kinaitwa Kasi Mpya Gold Mining Cooperative Society, kiliomba leseni eneo la Mwazimba; na kikundi kinaitwa Bushimangila and Masabi and Segese Gold Mining Cooperative Society (BMS) waliomba eneo la Bushimangila, Mheshimiwa Waziri ulifika; walishaomba leseni kwa taratibu zote. Kwa bahati mbaya sana utoaji wa leseni katika maeneo haya umekuwa na matatizo; na Mheshimiwa Waziri ulishaagiza amesema Mheshimiwa Musukuma hapa; katika vita tuliyonayo ya kupambana na ufisadi na rushwa moja ya maeneo ambayo tunayo bado ni kwenye Maafisa wetu wa madini. Afisa Madini Mkaazi wa Kahama, baada ya kuwa umeshaagiza siku mbili baadaye aliondolewa; akaja Afisa Madini mwingine, kazi yake ya kwanza aliyoifanya ni kutoa leseni kwa mtu mwingine ambaye wala hakuwa katika maombi ambayo tulikuwa tumeshakuomba na ulishaelekeza.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri kwa sasa hivi tayari pale kuna mgogoro, kwa sababbu kuna leseni ambayo imeshatolewa na ulishaagiza kwamba wale watu wapewe leseni lakini hamna kilichofanyika. Nilikuwa naomba sana, mgogoro wa leseni wa Mwazimba, mgogoro wa leseni wa Bushimangila leo utusaidie angalau kauli itoke kwa sababu kule tunategemea wananchi wangu watafurahi wakisikia kauli yako na msimamo wa mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni la kuomba wachimbaji hawa wadogo wadogo ambao wamewezeshwa kwa kiasi kikubwa sana wanamatatizo ya kupata hasara kwa sababu wanachimba kwa kubahatisha sana. Mbinu tunzozitumia sisi za kienyeji hizi za kupiga ramli hazitusaidii kujua mahala ambapo dhahabu ipo. Kwa bahati nzuri maeneo mengi ambayo sasa hivi wanaachiwa ni yale yaliyofanyiwa exploration na makampuni makubwa na data zimetunzwa na makampuni lakini copy ziko Wizarani. Tulikuwa tunaomba takwimu hizi ziwe shared na hawa wachimbaji wadogo wadogo ambao wanapewa leseni ili waweze kujua exactly mashapo yako wapi na waweze kuchimba with a focus kuliko huu uchimbaji wa kubahatisha bahatisha; tutaweza kuokoa hasara wanazopata, lakini tutaongeza tija katika shughuli zao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, naomba kusema naunga mkono jitihada za Serikali, naunga mkono bajeti hii, ahsante sana kwa nafasi.(Makofi)