Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Jumanne Kibera Kishimba (2 total)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA aliuliza:-
Hospitali nyingi nchini ikiwemo zilizo katika mji wa Kahama zina upungufu mkubwa wa vifaa tiba kama x-ray na ultra-sound. Nchi ya Kenya baada ya kutambua changamoto ya upungufu wa vifaa tiba ilitunga sera kuhusu kampuni binafsi kuingia ubia na hospitali kununua vifaa tiba na kugawana mapato yanayotokana na vifaa hivyo.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuiga mfano huo mzuri wa Kenya ili kunusuru maisha ya wagonjwa wetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jumanne Kibera Kishimba, Mbunge wa Jimbo la Kahama Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya inatambua modules mbalimbali na Serikali inaendelea kuangalia ni kwa jinsi gani inaweza kuzitumia katika eneo hilo. Aidha, Serikali inaendelea kununua vifaa na vifaa tiba na kusambaza katika vituo vya kutolea huduma za afya kulingana na uhitaji wa eneo husika. Sanjari na hilo, tunaendelea kuangalia mikataba hii ya kampuni binafsi ni kwa jinsi gani tunaweza kuichukua na kuitekeleza katika kusaidia upatikanaji wa vifaa na vifaa tiba katika hospitali na vituo vyetu vya kutolea huduma za afya hapa nchini.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y. MHE. JUMANNE
K. KISHIMBA) aliuliza:-
Mfumo wetu wa elimu unaonekana kuchangia mfumuko wa matatizo ikiwemo kujenga mazingira ya udanganyifu na wizi wa mitihani hali inayopelekea baadhi ya wanafunzi kufutiwa matokeo.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kumpima mwanafunzi kwa kutathmini tangu shule ya msingi na kuoanisha na mtihani wake wa mwisho ili kupata uhalisia na uwezo badala ya kumpima mwanafunzi kwa kigezo cha mtihani wa siku moja?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jumanne Kibera Kishimba, Mbunge wa Kahama Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa tathmini unaotumika kwa sasa unajumuisha alama za upimaji wa mwanafunzi awapo shuleni yaani alama za upimaji endelevu pamoja na mtihani wake wa mwisho. Mfano, katika matokeo ya mtihani wa mwisho wa kidato cha nne, kidato cha sita na ualimu yaani cheti na diploma, alama za upimaji wa mwanafunzi awapo shuleni zinachangia asilimia 30 na mtihani wa mwisho unachangia asilimia 70.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kufanya utafiti zaidi kwenye mifumo ya utahini inayotumika katika nchi mbalimbali duniani kwa lengo la kuboresha mfumo wa utahini kwa kadri inavyowezekana na inavyoonekana inafaa na kwa kuzingatia mazingira ya utoaji wa elimu bora nchini. (Makofi)