Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. George Boniface Simbachawene (79 total)

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini napata mashaka na majibu yake, kwa sababu hivyo vikao vyote vya ushauri vya DCC na RCC vimeshafanyika na nina uhakika kabisa Serikali hii ina taarifa ya maombi ya watu wa Morogoro Vijijini kuhamia kule Mvuha.
(a) Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba kwa sababu mchakato huu ulianza tangu mwaka 2009 wakati huo Mbunge akiwa Mheshimiwa Hamza Mwenegoha na Serikali hii imeshaleta shilingi milioni 500 kwa ajili ya maandalizi ya kuhamia Mvuha; hizo hela zimetumika kwa ajili ya udongo na kupima viwanja. Sasa leo Serikali inapokuja kusema haina taarifa, napata mshangao kidogo.
Mheshimiwa Spika, swali langu, sipendi kuidhalilisha Serikali yangu, namwomba Mheshimiwa Waziri arudi akatafute majibu sahihi ili aniletee kwa ajili ya maendeleo ya watu wa Morogoro Vijijini.
(b) Ni lini Serikali italeta majibu hayo sahihi ili tuweze kuwapelekea watu wa Morogoro Vijijini?
Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE - WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAMISEMI): Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri, Mheshimiwa Jafo, naomba kujibu swali ambalo hakupenda lijibiwe la Mheshimiwa Mgumba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli wanaweza wakawa wamefanya huo mchakato wote; lakini kama wameufanya na ukawa na dosari kama hizi zilizoelezwa kwa vigezo hivi, haukuweza kupita na kufika katika hatua zilizofuata. Nafahamu walikwama wapi, ndio maana hakijaanza kitu chochote.
Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumwagiza Mkuu wa Mkoa wa Morogoro waanzie pale walipoishia ili watuletee kwa sababu walipokwamia nafahamu siyo mahali pagumu sana. Wakirekebisha yale ya kwao, watuletee sisi tuone ili tuendelee na hatua zinazofuata. (Makofi)
MHE. TUNDU A. M. LISSU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kuhusiana na tatizo la Madawati. Mwaka 2015 tuliletewa taarifa na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI kwamba kila Halmashauri ya Wilaya ya nchi hii imepelekewa madawati siyo chini ya 708 yaliyotokana na chenji ya rada iliyotoka Uingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri yangu ya Wilaya ya Ikungi haijapata dawati hata moja. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri atueleze, madawati 708 ya Halmashauri ya Ikungi yalipelekwa wapi?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA (MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE): Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua upungufu wa madawati hasa zaidi kwenye Shule za Msingi na hata Sekondari. Serikali katika jitihada hiyo, tulianza kuamua kama Taifa kuhakikisha kwamba tunaondokana na tatizo la watoto wetu kukaa chini. Pia tukapata fursa inayotokana na fedha ya chenji ya rada ambayo Mheshimiwa amejaribu kuuliza na madawati yametengenezwa na baadhi ya Halmashauri nchini zimepata. Nakumbuka nina shule zangu kama mbili ikiwemo Shule ya Msingi Malolo, imepata.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA (MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE): Sasa kwa sababu Mheshimiwa ameitoa hii taarifa, tutajaribu kuangalia tupitie tuweze kuona kwa nini kama alikuwa yupo kwenye mgawanyo wa yale madawati katika Jimbo lake, hayakuweza kufika na yako wapi? Siyo rahisi kupata jibu la moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Serikali tunatambua hili na tumejipanga. Tunataka kuhakikisha kwamba ndani ya muda mchache sana ujao tunakuwa na madawati kwa nchi nzima. Nitakuja na Mpango na Maelezo, nitaomba Waheshimiwa Wabunge wote mniunge mkono.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa dhana ya kuhakikisha Serikali inadhamini kutoa elimu ni jambo la msingi. Tatizo lililopo sasa ni miundombinu katika shule nyingi. Jimboni Vunjo tuna shule zaidi ya 16 ambapo nyingine hazina vyoo na matatizo makubwa kweli, ambapo ni janga hata zile shule kuendelea kufanya kazi sasa kwa sababu zinaweza ikasababisha majanga makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiweka utaratibu ukaufuata inakuwa ni jambo jema. Serikali haioni umuhimu wa kuleta mini budget ili Bunge liweze kutekeleza wajibu wake ili fedha hizo ziumike kwa utaratibu ambao tumejiwekea Kikatiba badala ya Serikali tu kusema inaagiza, inapeleka huku, inapeleka huku, kwa utaratibu ambao haueleweki na unaoleta utata?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA (MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE): Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa najaribu ku-pause wazo zuri, kubwa na lenye mtazamo mpana. Hata hivyo Serikali imeanza kutekeleza mpango ule wa kuhakikisha kwamba tunatoa elimu ambayo hailazimishi wazazi na hasa maskini kutoa mchango ndipo mtoto aende shule. Hili kusema ukweli ukilitafsiri kijuu juu utaliona ni jepesi, lakini unapomzungumzia maskini, Serikali hii ya awamu ya tano imeanza kujaribu.

Mheshimiwa Spika, tumejaribu kuji-confine kwenye bajeti ya mwaka 2015/2016, maana kwenye bajeti hiyo kuna fedha iliyotengwa na Bunge, lakini kuna ile fedha iliyopatikana. Sasa tumejaribu kucheza kwenye ile difference. Mheshimiwa Rais akasema, basi tuanze kutoa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa shule inayoitwa capitation, itolewe in full amount kama ilivyokuwa imepitishwa siku za nyuma shilingi 10,000/= ambapo shilingi 6,000/= itaenda kwa ajili ya kila mtoto shuleni na shilingi 4,000/= itawekwa pamoja kwenye Wizara na kununua vitabu na kuwagawia, kupeleka kwenye mashule. Tumeondoa ile ya kununua vitabu kila mtu anakotaka.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali imefidia ada ambapo kwa Shule za Kutwa ni shilingi 20,000/=. Ilikuwa ni lazima kila mtoto, mzazi achangie; imefuta! Pia shilingi 70,000/= kwa watoto wa bweni, Serikali imefuta, imechukua huo mzigo. Pia tutapeleka fedha ya chakula shilingi 1,500/= kwa kila mtoto wa shule za bweni na Shule Maalumu za Msingi. Hizi zote kusema ukweli zilikuwa haziendi vizuri, sasa tunazipeleka kabla ya mwezi. (Makofi)

Vilevile tutapeleka fidia ya mitihani. Mtakumbuka, kila mtoto hasa wa sekondari kidato cha nne alikuwa analipia Sh. 50,000/= kwa ajili ya mitihani. Hizi Serikali itazilipa yenyewe kwenye Baraza la Mitihani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali hii imejipanga kutumia shilingi bilioni 18.77 kwa kila mwezi. Kwa hiyo, nikijibu na swali la rafiki yangu pale ni kwamba fedha hii ni kila mwezi. Hivi sasa tunajiandaa kupeleka nyingine.

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza tu changamoto ya idadi ya wanafunzi na records zilizokuja, ndiyo maana fedha zimeenda vibaya, lakini uzoefu tulioupata kwa mwezi huu, sasa naamini mwezi unaokuja tunaweza tukarekebisha hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubaliana suala la miundombinu kwamba ni changamoto, lakini tumeeleza wajibu wa Serikali, lakini tukaeleza pia wajibu wa wadau wa maendeleo na wazazi katika masuala mazima ya kuhakikisha kwamba Taifa letu linatoa elimu iliyo bora na ambayo ni nzuri na ya kueza kufanya Jamii yetu iweze kubadilika na ku-meet viwango vinavyotakiwa. Ahsante sana.
MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa msingi wa ahadi ya Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kutazama uwezo wa Halmashauri, kwamba haina uwezo wa kujenga madaraja haya pamoja na barabara zake, thamani ya madaraja haya mawili ni zaidi ya milioni 800.
Je, Waziri yupo tayari kuthibitishia Bunge lako na wananchi wa Jimbo la Nzega kwamba miradi hii itapalekwa TANROAD kama ambavyo Rais aliahidi?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikubaliane na yeye kwamba kwa kulinganisha na bajeti zetu za Halmashauri, fedha hii tu peke yake inaweza ikawa ndiyo bajeti ya Halmashauri hiyo kwa mwaka mzima kwa barabara zote. Kwa hivyo ni kweli kama anavyosema Mbunge na ndiyo maana pengine Mheshimiwa Rais alisema madaraja haya yapelekwe TANROADS.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Serikali ni moja, na ahadi iliyotolewa fedha zinatoka zote Hazina, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa dhana ya D by D hata kama Halmashauri haina uwezo ama wa kitaalamu au wa kifedha, kazi ya Wizara yangu ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ni coordination ambapo Wizara nyingine pia zozote zile zinaweza zikachangia ama rasilimali fedha au watu au ujuzi katika kuhakikisha kwamba Halmashauri zinafikia malengo yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, hili Mheshimiwa Mbunge lisimpe shida, ndani ya Serikali tutaangalia kama linafaa kufanywa hivyo basi tunaweza tukashirikiana na Wizara ya Ujenzi kuona namna ya kutekeleza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Waziri unafahamu kwamba gawio la Halmashauri za Mfuko wa Barabara ni ndogo sana zinazoenda kwenye Halmashauri zetu, tatizo la barabara siyo la Nzega tu lipo kwa nchi nzima baada ya mvua kunyesha sana mwaka huu barabara nyingi zimeharibika na madaraja. Napenda kufahamu Mheshimiwa Waziri kama upo tayari kuzungumza na Wizara ya Ujenzi ili gawio la Halmashauri ya fedha za Mfuko wa Barabara ziongezeke badala ya hivi sasa Halmashauri zimeshindwa kutengeneza barabara hizo zikiwemo za Babati Mjini?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba gawio ambalo Halmashauri zinapata kama fedha kwa ajili ya matengenezo ya barabara zetu hazina uwezo wa kuhimili mambo ya dharura. Kwa maana hiyo, kweli ipo haja ya kutafuta nguvu ya ziada katika kuhakikisha kwamba kwa dharura za mvua hasa zilivyokuwa nyingi kwa mwaka huu, basi tunapata fedha ili tuweze kukarabati hizo barabara lakini pia kutokuathiri miradi yake ya kawaida iliyokuwa imepanga na Halmashauri katika maombi yao ya fedha za kibajeti. Kwa kufanya hivyo ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge Wizara ya Ujenzi mara nyingi imekuwa ikitengewa fedha kwa ajili ya dharura hiyo ambayo kusema kweli inaweza isitoshe, lakini pale kunapokuwa kuna dharura kubwa tunachukua hatua na wanatoa fedha na tunaweza kutengeneza barabara hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kama dharura hiyo itakuwa ni kubwa kama ninavyoisema basi Serikali haitasita kufanya hivyo.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile fedha za Mfuko wa Barabara ni asilimia 30 kwa TAMISEMI na asilimia 70 kwa Serikali Kuu, hatuoni kutokana na mahitaji kama haya ya makorongo aliyoyasema Mheshimiwa Bashe, sasa wakati umefika wa kugawa fedha hizo asilimia 50 kwa 50 na Wilaya ya Hanang‟ ina makorongo makubwa kutokana na uharibifu wa mazingira lakini Halmashauri kama alivyosema Mheshimiwa Waziri haina uwezo kabisa wa kujenga makorongo hayo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba, Mfuko wa Barabara unagawanywa kwa asilimia maana mfuko ni mmoja, lakini Wizara ya Ujenzi inayoshughulikia barabara kwa maana TANROADS wanachukua asilimia 70 na Halmashauri zinachukua asilimia 30.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anajaribu kusema hapa kwamba, kwa sasa ni kama vile tunahitaji kuongezewa nguvu kwenye Mfuko wa Barabara katika upande wa barabara zinazosimamiwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa takribani ni sawa kwa sawa na zile barabara za Kitaifa zinazounga Mikoa kwa Mikoa kwa sababu uharibifu mkubwa umetokea zaidi huko.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni la kisera na kwa hivyo siyo rahisi kulitolea jibu hapa, lakini sichelei kukubaliana na yeye kwamba kweli kwa sasa iko haja ya kuangalia kama tunaweza kubadilisha hizi namba hata angalau tukafika asilimia 40, sasa hili ni jambo la kisera siwezi kuliamua peke yangu hapa kusema ndiyo au hapana, Serikali tumesikia tuendelee kulitafakari tuone kama kuna haja ya kufanya hivyo.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu ambayo Serikali imetoa ya hatua ya awali ya ujenzi wa hospitali ya Mkoa.
Swali langu la msingi nimeuliza kwa kuwa, hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda ndiyo iliyobeba uzito wa kuhudumia takribani wagonjwa zaidi ya laki tano wanaotumia bajeti ya Halmashauti ya Wilaya ya Mpanda, ni lini Serikali itaharakisha mchakato wa ujenzi huo wa hospitali ya Mkoa ili kuepusha Halmashauri ya Mpanda inayotumia bajeti ya Halmashauri kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wengi kinyume na utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuisaidia hospitali hii ili iweze kukidhi mahitaji kwa sasa?
Lakini swali la pili…
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili naomba kuweka uzito, tunavyo vituo vya afya ambavyo kama vingeimarishwa vingesaidia sana uzito wa hii hospitali ambayo imeelemewa. Serikali ina mpango gani wa kuviboresha vituo vya afya ambavyo vipo katika Mkoa wa Katavi, hususani vile vya Karema, Mwese na Mishamu, napenda kujua hayo.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ameuliza ni lini hospitali hii ya Mkoa itakamilika kwa sababu hospitali ya Mpanda ambayo ni ya Wilaya sasa ndiyo inayotumika kwa ajili ya kutoa huduma hizo za Kimkoa. Je, ni hatua gani za dharura ambazo Serikali inaweza kuzichukua kwamba tutajaribu kuona na kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda namna ambavyo tunaweza tukaiongezea uwezo wa dharura hiyo hospitali ya Wilaya ili kuweza kumudu majukumu ya Kimkoa. Hata hivyo, bado narudia kusema jibu la suluhu ya kudumu katika jambo hili ni kuhakikisha kwamba tunajenga hospitali hii na ndiyo maana Serikali inaendelea kutenga fedha kwaajili ya kujenga hospitali ya Mkoa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ameuliza je, kama kuna vituo vya afya ambavyo vinaweza vikasaidia kupunguza uzito huu wa wagonjwa katika hospitali hii ya Wilaya ambayo sasa inatumika kama hospitali ya Mkoa. Ni kweli Serikali tumejipanga na tutajaribu kuona kwa vipaumbele na kwa maeneo
aliyoyasema kama tunaweza tukaanza na vituo hivyo kutokana na bajeti iliyotengwa kwa ajili ya Halmashauri ya Mpanda.
MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru. Mheshimiwa Waziri hospitali yetu ya Wilaya ya Siha haina wodi ya watoto wala ya wazazi na hii inasababisha msongamano mkubwa sana katika hospitali yetu ya Mkoa ya Mawenzi.
Je, ni lini fedha hizo zitatoka ili ujenzi huo uanze mara moja?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, sikumsikia amesema hospitali ipi?
MHE. GRACE S. KIWELU: Hospitali ya Wilaya ya Siha.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki nisiamini kwamba kweli hakuna wodi kwa ajili ya watoto na wazazi na kama kweli hakuna basi ni jambo ambalo linahitaji udharura wa hali yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mipango mingi ya vipaumbele katika sekta mbalimbali za huduma za jamii inapangwa kenye Halmashauri zetu. Kwa hivyo, tutajaribu kuona ni kwa namna gani wamepanga vipaumbele vyao na kwa sababu bajeti ya Wizara yangu imeshapitishwa na kwa maana ya Halmashauri zote nchini, basi tuweze kuona tunaweza tukaanza na hivi ambavyo ni muhimu zaidi katika sekta ya afya, kwa sababu kweli ni jambo gumu kidogo kuonekana kwamba hakuna wodi kwa ajili ya watoto na wazazi katika hospitali ambayo ina hadhi ya kuwa hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, nitalichukulia very seriously na kulishughulikia jambo hilo.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Kituo cha afya cha Kirando kilianzishwa miaka 42 iliyopita wakati Kirando ikiwa ni Kijiji, leo kina wakazi mara 50 zaidi kutoka miaka 42, aliyekuwa Waziri wa Afya Mheshimiwa Dkt. Seif Rashid alifika pale Kirando na akaniahidi kwamba hiki kituo kweli kimezidiwa na ninafanya mpango wa kuwa hospitali kamili.
Lini Serikali yako itaipa hadhi kituo cha afya Kirando kuwa hospitali kamili kwa kuwa kimezidiwa na wagonjwa?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli inawezekana kabisa kwamba katika huduma za vituo mbalimbali vya afya kumekuwa na kuzidiwa kwa sababu ya umbali kutokana na maeneo yetu kati ya kituo kimoja hadi kingine. Lakini kwa
suala la kituo cha afya ya Kirando ambacho Mheshimiwa Mbunge anasema kwamba kimezidiwa na je ni lini au kuna mikakati gani ya kuimarisha ili kiweze kutoa huduma hiyo au kubadilishwa kuwa hospitali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kikubwa hapa ni ushirikiano kati ya mamlaka ya Serikali za Mitaa ambapo Waheshimwia Wabunge ni Madiwani kule katika kupanga vipaumbele vyetu, ni vizuri mkawa mnaturahisishia kazi ya kupanga halafu mnajua kabisa kwamba hatua zile huwa ikitoka pale mnaenda kwenye Mkoa ambapo mnashauriana, katika Sekretarieti ya Mkoa kwenye kikao cha ushauri cha Mkoa pale ndipo ambao mnaweza mkaja na mapendekezo halafu Serikali Kuu tukaona tuanze na lipi katika eneo lenu.
Mheshimiwa Ally Keissy, nikuombe tu kwamba kama mtasema tukiimarishe hiki na kuwa hospitali, basi jambo hili lije kwa utaratibu wa kisheria kama ulivyoelezwa katika Sera ya Afya.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba, posho za Madiwani kwa maana ya vikao na posho za Wenyeviti wa Mitaa, Vitongoji na Vijiji zinalipwa na Halmashauri na kwa kuwa Serikali imekiri kabisa kwamba wanatambua kuna Halmashauri zingine hazina uwezo, makusanyo ya ndani ni madogo kama ilivyo Halmashauri ya Mji wa Tarime.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini sasa Serikali isione ni vema mathalani kwenye vikao vya Madiwani ambavyo tumeona vinatofautiana kati ya Halmashauri moja na nyingine, wengine wanalipwa 60,000, wengine 80,000 wengine 250,000 wengine 300,000, kwa nini wasi-standardize iwe kama tunavyolipwa posho Wabunge kwa Tanzania nzima na iweze kutenga fedha, isitegemee mapato ya Halmashauri ili Madiwani wanavyokaa vikao vyao waweze kulipwa fedha ambazo ni uniform kwa Tanzania nzima, vilevile kwa Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kuhusuiana na suala la Wenyeviti wa Mitaa na Vitongoji na Vijiji. Tumeshuhudia wananchi wakienda kupata huduma majumbani kwao. Serikali inajibu kwamba, inategemea mapato ya Halmashauri. Narudi pale pale tuna Halmashauri zingine mapato ni madogo sana na haiwezi kujenga Ofisi za Wenyeviti. Kwa mfano, kwangu Halmashauri ya Mji tuna Mitaa 81 Halmashauri ya Mji wa Tarime haiwezi ikajenga hizo ofisi. Kwa nini sasa Serikali isione umuhimu kuwapatia hawa Viongozi ofisi zao iwajengee, itenge fungu kutoka Serikalini ishuke chini kwenye Halmashauri zote nchini iweze kujengewa ofisi ili kuepuka adha ambayo inaweza kupelekea hata wengine kushawishika na kutoa na vitu vingine?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vitongoji lakini pia Wenyeviti wa Vijiji wanafanya kazi nzuri sana na kila mmoja anajua. Lakini pia ndiyo ambao wanazisaidia sana hizi Halmashauri katika kutekeleza shughuli zake ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa hayo mapato yenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, itakuwa ni jambo la kusikitisha na linashangaza na tutachukua hatua kali sana kusema ukweli kwa Halmashauri zote ambazo hazitaheshimu formular ile ya asilimia 20 ya mapato ya ndani kuzipeleka kwa hawa watu muhimu sana wanaowasaidia katika kutekeleza miradi lakini pia kukusanya mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali itahakikisha inalisimamia jambo hili, lakini tusaidiane Waheshimiwa Wabunge ninyi ndiyo Wajumbe wa Halmashauri zenu huko. Haya yanafanywa na watu ambao wako chini yenu kabisa kinidhamu, kwahiyo ni vizuri tukasikia huko mnachukuliana hatua kwa sababu mna hiyo mamlaka na sisi tukaja kusaidia pale tu ambapo huyu mtu amekuwa ni tatizo sugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vigumu pia kuweka standard formula na standard formula tulioiweka kama Serikali tumesema ni asilimia 20 ya mapato ya ndani, kwa sababu kwanza kabisa ili uweze ku-establish Halmashauri lazima vigezo kadhaa uweze kuvifikia ikiwa ni pamoja na hali ya uchumi wa eneo husika. Sasa tulipokuwa tunaomba Halmashauri, tunaomba tu ili tuweze kuzipata, lakini tunakuja kupata shida pale inapokuwa vigezo vile tulivyovisema siyo halisi kwa sababu huko kiwango cha uwezo wa ndani ndiyo unao-determine uanzishwaji wa Halmashauri husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi naamini kwa Halmashauri zilizoanzishwa na kama kweli zilikidhi vigezo vilivyopo kwa mujibu wa sharia, basi haziwezi zikashindwa kabisa kuweza kuwalipa posho hawa watu muhimu sana katika ngazi ya Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Mitaa. Kwa sababu hawa watu kama nilivyosema ndiyo wanaosaidia kukusanya mapato hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili juu ya ofisi za Viongozi hawa muhimu ni kweli tungeweza kusema ni jambo zuri kwamba nchi nzima tukawa na utaratibu wa kujenga ofisi hizi zote, lakini kama mnavyofahamu bajeti yetu ni hiyo moja na kupanga ni kuchagua, ndiyo maana tumeziachia Halmashauri kwa dhana ya kupanga vipaumbele vyao, basi kama kipaumbele cha Halmashauri fulani ni ofisi hizi tunaweza tukaanza na hizo na sisi Serikali Kuu tutatenga kwenye bajeti yetu kwa kadiri ya sealing ilivyopangwa kuhakikisha kwamba, tuna-facilitate au tuna-fund miradi ambayo imeibuliwa kutoka huko chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni jukumu la Halmashauri kuhakikisha kwamba kutokana na makusanyo yao ya ndani ambayo hayana masharti kutoka Serikali Kuu, basi wanapanga kupunguza upungufu huo wa ofisi kila mara wanapopanga katika bajeti zao.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa watu wenye ulemavu na hasa wanafunzi, wengi wao wanatoka katika familia duni na changamoto ni nyingi:-
Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kutoa nafasi ya kipekee na ya upendeleo kwa watoto hawa wenye ulemavu, wale wanaobahatika kwenda Kidato cha Tano na cha Sita ili waweze basi kusoma bure kama walivyosoma katika elimu ya Shule ya Msingi na Sekondari?
Swali la pili, pia baadhi ya wazazi, walezi na hasa katika baadhi ya jamii zetu, huwatenga na kuwaficha watoto wenye ulemavu kwa kuwaona kuwa ni mkosi na kuwakosesha haki yao ya msingi ya kupata elimu:-
Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya wazazi au walezi wenye tabia hizi wanaokosesha watoto kupata elimu kwa sababu tu ya ulemavu walionao? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba ni jukumu la jamii kwa ujumla kwa maana ya Serikali, wananchi wote na wadau, wakiwemo wazazi na walezi wa watoto na mamlaka zao za Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba watoto hawa wanapata nafasi ya kipekee ili waweze kupata elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika utaratibu wa sasa, tumeamua kufanya kazi hiyo kwa kusaidia wale wanaoanza kuanzia chekechea, Shule ya Msingi naKkidato cha Kwanza hadi cha Nne. Kwa Kidato cha Tano na cha Sita, utaratibu huu mara nyingi tunatambua huwa unafanywa chini ya Wakuu wa Wilaya ambao hushirikiana na Halmashauri katika kuwabaini wale ambao hawana uwezo na kuweka utaratibu wa kuwasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, tufahamu kwamba unapozungumzia dhana ya D by D ni pamoja na kubeba majukumu kama haya ambayo hayana utaratibu wa moja kwa moja wa kimfumo wa kibajeti. Pale kwenye Halmashauri, Mkurugenzi kazi yake siyo tu kuangalia mambo ya jumla ya kila siku ambayo yanafanywa kwa maana ya Idara zile, lakini pia kwenda zaidi na kuona jukumu lla kubeba jamii yote kwa ujumla, wakiwepo hawa wenye ulemavu na watu wengine wenye mahitaji maalumu kuhakikisha kwamba na wao wanapata haki zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivi, Mkurugenzi huyu anashauriwa na Baraza la Madiwani ambalo lipo kwa ajili la uwakilishi wa wananchi kama hawa. Kwa hiyo, nina hakika hili jambo limekuwa likifanykia na hawa wanafunzi wanaohitaji nafasi ya kupata elimu kwa sababu ya mahitaji maalum na wale tu wasiokuwa na uwezo hata kama siyo walemavu wamekuwa wakisaidiwa na mamlaka hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwamba kumekuwepo na tabia ya baadhi ya jamii kuwatenga watu wenye ulemavu wasipate haki zao za msingi; tulipotunga sheria mwaka 2010, katika kifungu cha 28 cha sheria ya watu wenye ulemavu, tumezungumzia juu ya haki mbalimbali, lakini pia tumeridhia itifaki mbalimbali za Kimataifa juu ya haki mbalimbali za watu wenye ulemavu.

MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba unisamehe tu, maswali yangu yatakuwa marefu kidogo kwa mara ya kwanza katika historia yangu ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Spika, nafahamu kabisa Mheshimiwa Naibu Waziri anachosema humu ndani ni majibu aliyoandikiwa kutoka huko huko kwenye matatizo, waliomwandikia ndiyo chanzo cha mgogoro huu. Sasa swali la kwanza; je, yuko tayari kwenda mwenyewe badala ya kusubiri majibu anayoandikiwa kutoka huko Kiteto?
Swali la pili, hivi sasa wapo wakulima kutoka Chemba, Kongwa, Kondoa na maeneo mengine ambayo wafugaji wameamua kwenda kuchunga mashamba yao wakati yakiwa na mazao shambani na hakuna chochote kinachofanywa na mamlaka ya utawala wa Kiteto. Je, kama ninyi Waheshimiwa Mawaziri mmeshindwa kutatua tatizo hili, mko tayari sasa kuturuhusu tumwombe Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli akamalize tatizo hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini kwamba majibu haya tumeandikiwa na hao hao ambao wamesababisha mgogoro huo ni tuhuma nzito na nataka nikubaliane na ombi la Mheshimiwa Mbunge la kwenda kuuona ukweli ukoje sisi wenyewe. Kwa hiyo, tutajitahidi, tutajipanga ili tuweze kwenda. (Makofi)
Pili, ni kwamba migogoro ya ardhi nchini ya mwingiliano kati ya shughuli za kilimo na shughuli za ufugaji inachochewa sana na maendeleo, kwamba wananchi sasa kila mmoja anatafuta namna ya kupata maendeleo. Hivyo sidhani kama kuna namna ya muujiza unaoweza kufanyika kuimaliza kama tu wadau wote, Serikali, wakulima, wafugaji, hawatatumia busara na hekima zilizokuwa zinatumika na wazee wetu wa zamani wakati hakuna hata sheria nyingi kama ilivyo sasa.
Mheshimiwa Spika, kuthamini mali ya mtu mwingine ni jambo jema sana. Kinachotokea sasa hapa ni watu kuacha maadili na utaratibu wa kimila na desturi zetu. Zamani huko ilikuwa migogoro kama hii wanaimaliza kule, lakini unapokwenda kule unakuta kuna makundi na wanaochangia wengine ni sehemu ya watu wanaotakiwa kutatua migogoro hiyo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sitaki nibishane na Mheshimiwa Mbunge hapa, ninachosema kesi zinatofautiana kati ya kesi moja na kesi nyingine, tutajaribu kwenda na tutakapokwenda tutajaribu kutatua tatizo hili kwa mazingira yake na kwa namna lilivyo.
Mheshimiwa Spika, lakini kusema ukweli, nikiri na nikubali kwamba liko tatizo kubwa na ni lazima sisi Serikali tulishughulikie na tuko tayari kufanya hivyo na nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba nitakapokwenda huko nitajaribu kushughulikia tatizo hili kwa namna lilivyo, bahati nzuri nalifahamu sana.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na namshukuru Mheshimiwa Waziri na nampa pole sana kwa ajali iliyompata.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ni kweli nia ya kupeleka maeneo ya kiutawala karibu na wananchi mambo yanaweza yakachochea maendeleo kwa upande mmoja, lakini vilevile yanaweza kupeleka huduma jirani na wananchi, lakini je, Serikali haioni kwamba kutokana na kukua kwa mahitaji ya shughuli za kimaendeleo katika nchi yetu utakuwa wakati muafaka kuangalia upya Sheria ya Ugawaji wa Mikoa, Wilaya na maeneo mengine ya kiutawala ili kuokoa fedha zinazopelekwa katika utawala kwenye bajeti ya Taifa na kuzielekeza zaidi katika bajeti ya maendeleo? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kufanya hivyo, huoni kwamba Serikali inaweza ikajikuta inapeleka zaidi fedha kwenye ujenzi kwa mfano wa hospitali, shule badala ya kujenga nyumba za watumishi ama za viongozi mbalimbali ambao wanaongezeka idadi na kuleta mzigo mkubwa kwenye bajeti? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama tulivyojibu katika jibu letu la msingi kwamba ugawanyaji wa maeneo ya kiutawala unazingatia sheria zilizopo hizi mbili, Sura 287 na 288 za Serikali za Mitaa lakini zinabebwa na msingi wa Katiba. Lakini pia kubwa ni ushirikishwaji na hitaji la wananchi kwa sababu hatugawi tu, tunagawa kwa sababu msingi wake ni kurahisisha huduma kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nikuoneshe takwimu; wakati Morogoro yenye ukubwa wa square kilometer 77,522.08 ni Mkoa mmoja, Kilimanjaro, yenye size 13,209 ni Mkoa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wakati Tabora yenye ukubwa wa size ya square kilometer 76763.03 lakini Kilimanjaro ina size hiyo. Lakini nyingine wakati Jimbo la Liwale tu lina ukubwa wa size ya square kilometer 34300.92 Hai ina square kilometer 1011. Tukisema kwamba tusiendelee kugawa, tukasitisha kama Mheshimiwa Mbunge anavyosema uwiano uko wapi katika kutoa huduma za wananchi? (Makofi)
Mheshimia Spika, mahitaji haya ya sheria kuangaliwa upya kwa msingi wa kusitisha pengine sio jambo la busara sana, pengine tufikirie kama nia ni kupunguza matumizi ya Serikali, kuunganisha hivi visehemu vidogo vidogo ili viwe sehemu moja, viwiane na maeneo mengine makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili hizo issue ni fedha, haya ndiyo matumizi ya fedha kwa ajili ya kuhudumia watu. Kwa hiyo hauwezi ukabanwa kwamba matumizi ya fedha, kwani zinatakiwa ziende wapi? Si ziende zikahudumie watu? Kwa hiyo swali la pili, Serikali itaendelea kutenga/kugawa maeneo haya kwa msingi wa mahitaji kwa kuzingatia Katiba na sheria zilizopo. (Makofi)
MHE. MARYAM S. MSABAHA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na pole sana. Mwenyezi Mungu ni mwingi wa rehma. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa nchi za wenzetu kama kwa mfano nchi za jirani South Africa na nchi nyingine wametenga maeneo kwa ajili ya mama lishe, maeneo rafiki na wanauza vyakula vyao bila kubughudhiwa.
Je, Serikali mna mikakati gani kuhakikisha mnatenga maeneo maalum kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wadogo hasa mama lishe?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Jafo, kwa majibu mazuri ya swali la msingi.
Mheshimiwa Spika, lakini nikuhakikishie tu kwamba Serikali inatambua mchango mkubwa katika uchumi wa nchi yetu kutoka kwa wafanyabiashara wadogo wadogo.
Hata hivyo Serikali imeweka mkakati na tumetoa waraka maalum kuwaagiza Wakuu wa Mikoa na Wilaya, kusimamia Halmashauri kutenga maeneo mahususi, maalum kabisa kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo wadogo. Na ndiyo maana Mheshimiwa Rais katika agizo lake la kwamba, wafanyabiashara wadogo wadogo hawa, wamachinga, wasibughudhiwe bali wasaidiwe. Ni agizo ambalo tunalitekeleza na tumeanza kulipa mkakati wa namna ya kulitekeleza.
Mheshimiwa Spika, lakini niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, wao ni Wajumbe wa Mabaraza ya Madiwani na wao ni Madiwani. Hawa mgambo wameajiriwa na Halmashauri zetu, hawa mgambo si sawa na polisi, kwa hiyo, hawawezi wakapewa kazi kubwa ya kufanya operation hivi kwenye Halmashauri, maeneo ambayo sisi tunayasimamia bila maamuzi ya vikao, bila kusimamiwa na wataalam au hata na kamati fulani ya madiwani wakaanzisha tu operation hivi.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunawapa madaraka makubwa ambayo hayastahili, sisi ndio wenye Halmashauri na hawa ni waajiriwa wa Halmashauri, lazima kila operation inayofanyika kwa nia nzuri ya kuwatoa watu ambao wanavunja mahususi ya Halmashauri, hakika ni lazima tuhakikishe kwamba tunasimamia zoezi hilo na si kuliacha likafanyika kiholela.
Mheshimiwa Spika, yanayofanyika mengi ni makosa ya sisi Halmashauri kuwaruhusu wale kuwa na mamlaka makubwa na kufanya operation bila kuwasimamia.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ningependa niulize swali langu moja.
Kwa kuwa fedha ambazo zinatolewa kwa hawa akina mama lishe na kufanya biashara ni fedha za Serikali ambao walio wengi zinatoka TASAF, ni fedha za kuondo umasikini. Na kwa kuwa sasa Watendaji wengi sana wa Vijiji hawajaajiriwa kwa hiyo wanafanya zile kazi kama kukomoa. Je, sasa Serikali inasemaje kuhusu hilo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba maeneo mengi vijijini Watendaji wa Vijiji na hata wa Kata, hawajaajiriwa kwa ajira rasmi na Halmashauri husika, na hii inapelekea utekelezaji wa shughuli za maendeleo ikiwa ni pamoja na uwajibikaji kuwa katika kiwango cha chini kwa sababu mtu anaona mimi sijaajiriwa kwa hiyo nikifanya lolote lile ni sawa tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumekubaliana na tulipitisha hapa utaratibu kuanzia mwaka jana, tumeruhusu kwamba kada fulani za chini zinaweza zikatolewa ajira hizo na mamlaka husika kutegemeana tu bajeti zao walizozitenga. Nitoe rai kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha kwamba zinatoa ajira za Watendaji wa Vijiji ambao kwa sifa na kwa utaratibu tulioweka wanaruhusiwa kuzitoa wao ili waweze kuwa wamekamilisha idadi ya vijiji na watendaji wote wakamilike wale walioajiriwa na Serikali itakuwa tayari kupokea isipokuwa tu wazingatie sifa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyo vyuo ambavyo vinatoa watu waliosomea masuala ya mamlaka ya Serikali za Mitaa na mifumo ya Serikali za Mitaa Tanzania, Chuo cha Hombolo ambacho kina wataalam wazuri sana tunacho Chuo cha Mipango, Dodoma ambacho nao wamefundishwa masuala haya ya mipango vijijini ni vizuri watu wanaoajiriwa wakawa wanatoka kwenye vyuo hivi.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na nishukuru pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo yaliyoko kwenye Jimbo la Makambako yanafanana sana na matatizo yaliyoko kwenye Jimbo la Nyamagana katika Kata za Kishiri na Igoma. Majibu ya Mheshimiwa Waziri ni mazuri sana ila nilitaka tu kupata uhakika kutoka kwake na sisi ambao tuna matatizo ya kupata huduma kati ya Kata ya Kishiri na Igoma tukirudia mchakato huu upya kuanzia kwenye ngazi zote ambazo amezitaja tukaleta kwake tutapata approval ya kufanya marekebisho kwa wakati? Nashukuru.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri Jafo, napenda niongezee kwenye swali la nyongeza lililoulizwa na Mheshimiwa Mabula kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na migogoro mingi ya mipaka ambayo kimsingi si yote inaitwa migogoro. Wakati mwingine kulitokea makosa wakati wa kutafakari mipaka hiyo na kugawanya mamlaka za utawala lakini wakati mwingine inatokana tu na mabadiliko ya kijiografia na mahitaji yameelekea upande ambao pengine busara sasa inataka namna mpya itizamwe ili kuweza kurekebisha mipaka hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu niwashauri Waheshimiwa Wabunge kwamba michakato hii kwa mfumo wa kisheria na taratibu zake inaanzia huko huko chini. Kama ninyi huko chini mtatoa kwenye vikao vyote vya Wilaya na Mkoa mkawa mmekubaliana sisi huku kubadilisha hizi GN si tatizo kubwa. Kwa hiyo, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge mkazitaarifu mamlaka na vikao vinavyohusika viweze kufuata taratibu za kisheria kama zinavyotaka na kama walivyopendekeza mpaka tukafikia kuweka mipaka hiyo, wafanye hivyo hivyo katika kupendekeza kama wanataka kubadilisha mipaka hiyo na sisi Serikali hatutakuwa na pingamizi katika jambo hilo.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Naomba niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa ajali nyingi zinasababishwa na baadhi ya madereva walio wazembe na mfano mzuri ni katika Jiji la Dar es Salaam katika utaratibu mpya ulioanzishwa kwa jitihada za Serikali wa mabasi yaendayo kasi; hadi sasa zaidi ya mabasi 30 yamepata ajali na gharama za matengenezo hayo ni zaidi ya shilingi milioni 90. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhakikisha kwamba kama ni sheria, zinawabana madereva wazembe wanaoisababishia Serikali hasara? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba baadhi ya madereva wakiwemo madereva wa pikipiki, bodaboda na magari binafsi na hata magari mengine tu kwa ujumla, bado sharti na sheria inayotaka wasitumie barabara ya mabasi yaendayo kasi inakuwa ngumu sana kwao na hivyo kusababisha ajali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kwamba barabara ile ni kwa ajili ya mabasi yaendayo kasi na siyo vinginevyo. Kwa hiyo, mtumiaji mwingine yeyote anayetumia barabara zile anakuwa amevunja sheria na hivyo, yeye ndiye amegonga yale mabasi na kusababishia hasara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli takwimu zinaonesha kwamba ajali ni nyingi, na sisi tunasema tutaendelea kusimamia sheria ili kuhakikisha wananchi wanapata elimu, lakini pia watambue kwamba kwa kufanya hivyo wanafanya makosa makubwa na kusababisha hasara. Hawaruhusiwi kutumia barabara za mabasi yaendayo kasi zinazotumika sasa kwa Dar es Salaam.
Kwa hiyo, nawaomba sana wakazi na watumiaji wa barabara Dar es Salaam, kuheshimu barabara za mabasi yaendayo kasi ili kuipunguzia Serikali hasara zinazojitokeza.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: nakushukuru sana dada yangu Mheshimiwa Naibu Spika na Mbunge wa Viti Maalum Kinondoni. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Wamachinga siyo eneo, ni mazingira ya biashara. Nimekuwa nalisema hili mara zote. Ndiyo maana tulikuwa wakati ule tukisafiri kwenda China, Beijing, mimi kazi ya kwanza naangalia mazingira ya Wamachinga, wapo hawapo? Unakuta wapo. Ukienda New York unaangalia Wamachinga; wapo? Unakuta wapo. Kinachotakiwa ni mazingira ya kibiashara.
Mheshimiwa Waziri, naomba ukae kidogo. Kwa ajili ya kuweka kumbukumbu sawasawa, mimi ni Mbunge wa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais, sio Mbunge wa Viti Maalum. Kwa hiyo, lazima kumbukumbu zikae sawasawa.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbilinyi, kwamba tatizo la wafanyabiashara wadogo wadogo wanaojulikana…(Kelele)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimemwelewa Mheshimiwa Mbilinyi kwamba Wamachinga tatizo lao siyo kuwajengea, ila tatizo lao ni mazingira yanayofaa kwa biashara zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami nataka nikubaliane naye kabisa kwa sababu Wamachinga hata ukiwajengea sehemu nzuri namna gani, kwa sababu wateja wa Wamachinga wanajulikana. Kama wateja wale hawafiki, ni kazi bure. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niziombe Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini, Mheshimiwa Rais amesema wasibugudhiwe hawa; maana yake nini? Watafutiwe maeneo yanayofaa kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge; yanayofaa kwa shughuli zao. Kwa hiyo, naweza kusema nimeelewa swali la Mheshimiwa Mbunge na kwamba Mamlaka za Serikali za Mitaa zinafahamu wajibu wao na zilikwishaelekezwa na Mheshimiwa Rais alikwishasema kwamba watengewe maeneo yanayofaa kwa shughuli zao.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Wilaya ya Longido imeanzishwa mwaka 2007, takribani miaka tisa mpaka leo Wilaya ile haina hospitali ya Wilaya, matokeo yake wagonjwa wakipewa rufaa, wanapelekwa, Mount Meru - Arusha, kiasi cha kilometa 94 na Serikali imekuwa ikiahidi itajenga Hospitali ya Wilaya. Tunataka majibu ya uhakika, ni lini Serikali itajenga Hospitali ya Wilaya ya Longido?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Wilaya ya Longido haina Hospitali ya Wilaya kama zilivyo Wilaya nyingine nyingi tu hapa nchini. Niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba miradi ya Halmashauri, inaanzia kwenye mipango ya Halmashauri na baadaye bajeti ya Halmashauri. Kwa hiyo, niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge kwamba kule kwenye mipango ya Halmashauri ndiko vitu hivyo vionekane ili baadaye vikija huku Bungeni tuweze kuvitengea bajeti kwa mujibu wa taratibu za kibajeti.
Mheshimiwa Spika, imekuwa ni kawaida mimi kupata wageni wanaoomba vitu nje ya bajeti. Uwezo huo sina na hata Waziri wa Fedha, nadhani hana. Bajeti ikishapitishwa ndicho kitakachofanyika. Hivyo, Wilaya ipange mipango yake, mipango hiyo iwemo kwenye bajeti za Halmashuari zao. Jambo kubwa litakalobakia sasa ni kwa Wabunge ku-demand utekelezaji wa bajeti ili tufikie yale malengo hilo la kwanza.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwasihi Waheshimiwa Wabunge, kwamba kwa sera ya Serikali ni kuweka kituo cha afya kila kata, lakini Serikali tumeamua na tumepanga na Wizara ya Afya kuhakikisha kwamba kila Halmashauri basi angalau ijenge kituo kimoja. Katika Halmashauri 185 tulizonazo, tukifanya tutapata vituo karibu zaidi ya 400, wakati toka uhuru tuna vituo kama 600 tu.
Mheshimiwa Spika, nadhani hii itatusaidia sana, wa-dedicate maeneo, indication kulingana na maeneo ambako kuna problem kubwa. Jambo lingine ni kwamba kwenye zahanati wananiomba ramani, ramani ile iliyotolewa na Wizara ya Afya tumekubaliana na Waziri wa Afya kwamba ni kubwa mno kwa zahanati kila kijiji na haitekelezeki kwa sababu ya gharama kubwa karibu ya 1.8 billion ili iweze kutekeleza ule mradi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumekubaliana ku-review ile bajeti, kwa sababu tuna zahanati ambazo zilijengwa wakati tulipopata uhuru tu, zilitosha kutuhudumia mpaka leo tupo. Kwa hiyo, tunadhani zisiwe kubwa kiasi cha kushindwa ku-manage uchumi wa kijiji kwa sababu sehemu kubwa ni michango ya wananchi itatumika pamoja na kwamba Serikali itaweka mkono wake, lakini lazima ramani iwe ya kawaida inayoweza kuwa manageable.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naitwa Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko.
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kabisa kwamba ukosefu wa nyumba za walimu na kukaa mbali na shule unasababisha kutokuwa na kiwango kizuri cha ufundishaji kwenye shule zetu. Hivi karibuni tulisikia kauli ya Waziri Mkuu akitoa msisitizo kwamba walimu waishi kwenye shule ambazo wanafundisha. Kwa majibu ya Naibu Waziri ni dhahiri bado Serikali haijawa na mpango madhubuti wa kuhakikisha walimu wanakaa kwenye maeneo ambayo wanafundisha.
Ni nini mpango mkakati wa Serikali hasa kwa pale ambapo wananchi wamejenga maboma wanashindwa kuyamalizia ili watoto wetu waweze kupata elimu mbadala kwa Walimu kukaa maeneo ya shule. Napenda kupata mkakati ambao unatekelezeka siyo wa kuandikwa tu kwenye makaratasi, ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza na kuongezea kwenye swali la msingi pia ambalo limejibiwa na Naibu Waziri vizuri kabisa, Mheshimiwa Jafo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna mahitaji makubwa ya madarasa, tuna mahitaji makubwa ya nyumba za walimu. Kwa mfano, tuna upungufu wa madarasa katika shule ya msingi kwa sasa 127,745. Tuna upungufu wa madarasa kwa shule za sekondari 10,204. Hali kadhalika tuna upungufu wa nyumba za walimu. Mipango yote, mpango uwe mpango mkakati, uwe mpango wa haraka, uwe mpango wa dharura, inafanyika kwenye Halmashauri zetu. Tusitegemee kwamba tutakuja na mpango fulani nje ya mipango ile ya Halmashauri, kwa sababu Serikali kwa mujibu wa Katiba, kwa mujibu wa sheria, tunatekeleza dhana ya ugatuaji wa madaraka.
Mheshimiwa Spika, kugatua madaraka maana yake ni kwamba tupange vipaumbele sisi tulioko huko kwa wananchi. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kwanza kuwapongeza sana wananchi wote wa Tanzania wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, kwa namna tulivyoshirikiana vizuri sana katika suala la kupunguza upungufu wa madawati. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo sasa, tuangalie namna ya kwenda kwenye mchakato wa kupunguza tatizo la nyumba za walimu na madarasa. Tukifikiri kuna njia nyingine nadhani tutakuwa tunajidanganya, ukweli ni kwamba lazima tujipange wenyewe kwa kutumia rasilimali zilizopo na ndiyo maana katika bajeti ya mwaka huu tunayoiandaa, msisitizo mkubwa ambao tumeelekeza Halmashauri sisi TAMISEMI ni kwamba wajipange sana kuweka fedha nyingi na mipango mikubwa kwenye madarasa na nyumba za walimu. Hii itatusaidia ili hata Serikali kama ikitoa fedha yoyote ile, itakwenda kwa njia hiyo ili kutekeleza upungufu uliopo.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya viongozi katika ngazi za Wilaya, hasa ma-DC na ma-DAS, wengi wao wamekuwa wababe na wamekuwa wakitumia madaraka yao kuwanyanyasa wananchi kwa kisingizio eti wao ni Marais wa Wilaya. Wakati nafahamu katika uchaguzi uliopita tumemchagua Rais mmoja tu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)
Je, Serikali haioni hili linaweza kuwa ni tatizo kubwa sana? Na inawezekana kama tutaendelea bila kufanya utafiti wa kutosha na kuwachunguza watu hawa wanaweza kuharibu hata imani ya wananchi kwa Chama cha Mapinduzi?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kama nilivyosema muda mfupi uliopita kwamba hawa ni binadamu na ni Watanzania wenzetu. Na kutokana na kazi na nature ya kazi wanazozifanya inawezekana mahali fulani kukatokea mikwaruzano, lakini tatizo la mtu mmoja haliwezi kuwa la watu wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanafanya kazi nzuri sana. Wanatusaidia maana wao ndio wasimamizi kwa niaba ya Serikali katika maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa jana lilitokea swali ambalo lilikuwa linataka kufahamu kofia au nafasi ya Mkuu wa Mkoa. Mkuu wa Mkoa ana kofia mbili, ana kofia ambazo zinashuka kwa Rais zile mbele, Head of Executive and Head of State. The President is Head of State and at the same time Head of Executive. Wakuu wa Mikoa wanashukiwa na zile kofia mbili na ndio maana wanalindwa na bunduki kati ya saba mpaka kumi na moja na askari saba hadi kumi na moja. Na ni haki yao wao kulindwa kwa sababu wanafanya maamuzi mazito, wanaweza wakaingilia jambo ambalo haliendi sawa kwa sababu ndio wawakilishi wa Serikali katika maeneo yao. Na kwa hiyo lazima vyombo vya ulinzi na usalama viwalinde kwa sababu ya nature ya kazi zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuwaomba sana Waheshimiwa Wabunge ni suala la mawasiliano, sio na ninyi tena kutunishiana ubabe kule. Kinachowezekana kutokea kule sasa ikiwa hivyo itaonekana nani ni nani. Lakini kama tukiletewa, inapotokea upungufu tunaweza tukashughulikia administratively tu na jambo likaenda vizuri, kama nilivyosema hawa nao ni binadamu. Kwa hiyo, pale ambapo tunapata fursa tumekuwa tukitoa maelekezo kwao na tumekuwa tukitoa hata kwa maelekezo ya maandishi na wala semina sio jambo la msingi sana. Lakini kubwa hapa ni maelekezo na mtu kujua wajibu wake.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, kwanza mimi na-declare my interest kwamba ni Mjumbe wa Kamati yako ya Kudumu ya Utawala na TAMISEMI. Kwa hivyo,
katika ziara zetu mbalimbali tumepata ushuhuda wa wanufaika wa kaya maskini na kiwango fulani wamenufaika kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na kunufaika kwao bado haijaondoa umuhimu wa kuweza kuongezewa hii ruzuku kwa sababu kama nilivyosema katika swali langu la msingi kila siku maisha yanapanda, shilingi yetu inaporomoka
na bei ya bidhaa inaongezeka. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri anaonaje basi wakaweza kupewa viwango hivi wanavyopewa kwa mkupuo walau wa miezi sita ili ile tija ya kuweza kuendesha biashara zao, kujenga makazi yao ikapatikana?
Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili dogo, mimi
nashukuru katika Jimbo langu pia mradi huu katika baadhi ya shehia unaendelea lakini kuna usumbufu wale walengwa kutoka katika vijiji vingi wanakusanyika katika center moja.
Waziri anaonaje akaongeza vituo vya kulipia ili wale watu ambao wamekusudiwa kupewa ruzuku hii wasipate matatizo hasa ukizingatia wengine ni wanyonge sana, wengine ni watu wazima mno…
Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, nimeeleza katika majibu ya swali langu la msingi. Kwanza kabisa, ukiangalia mradi huu, kabla hatujaanza uhawilishaji mwaka 2013 tulianza mpango wa majaribio mwaka 2008 kwa miaka mitano katika Halmashauri tatu za Chamwino, Bagamoyo pamoja na Kibaha. Katika mpango huo wa majaribio, kaya 26,000 zilishiriki katika mpango huu.
Mheshimiwa Spika, ukiangalia mwanzoni wakati
programu inaanza, wakati huo wa majaribio, kiwango cha juu kabisa kilikuwa ni Sh.17,500/=. Hata hivyo, tulipoanza mpango tulipandisha mpaka Sh.34,000/= na ilikuwa haiangalii watoto walioko katika kaya, haingalii watoto wanaopata huduma za kiafya na zinginezo. Nipende tu kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeongeza, kwa sasa hivi kiwango cha juu kabisa ni Sh.76,000/= vilevile wanapata fursa pia ya kupata ujira, kwa siku 60 kila mwaka wanapata takribani Sh.138,000 kwa Sh.2,300 kwa siku.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kusema
kwamba katika majaribio ilionekana ukiwapa kiwango kikubwa sana inawezekana wakabweteka na wasiweze kufanya shughuli zingine za ujasiriamali na wakajitegemea tu kupitia ruzuku hii. Kwa hiyo, ilionekana kwa kweli kiwango hiki kinafaa na tumefanya majaribio na wako wengi ambao wameweza kunufaika na kupata maendeleo katika maishayao.

Mheshimiwa Spika, katika swali lingine kwamba
wapewe sasa kwa mkupuo wa miezi sita, hoja yake Mheshimiwa tunaiona, napenda tu kusema kwamba tunaendelea kuifanyia kazi ili kuona kama inawezekana miezi sita au miezi mitatu na nini kinaweza kikafanyika. Kwa sasa nisiseme kama tumekubali, lakini niseme tunaona hoja ni ya msingi tuichukue twende tukaifanyie kazi.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hoja ya kuongeza vituo vya kulipia fedha na yenyewe pia niseme tunaichukua ili kuona ni kwa namna gani tunaweza tukawarahisishia na kuwasogezea huduma karibu zaidi walengwa wetu.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa kila Halmashauri ya Wilaya ina Mratibu wa TASAF na waratibu ndiyo wameandikisha kaya
maskini, walijua kabisa kwamba kaya hii ni maskini. Hivi
karibuni kuna kaya ambazo zimeondolewa kwamba hazina sifa na wanaambiwa warejeshe fedha, wengine ni wazee kabisa. Mheshimiwa Waziri nani mwenye makosa, ni mratibu aliyeorodhesha au ni yule ambaye ameambiwa kwamba alipe hizo fedha?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia utekelezaji mzima wa mpango huu, lakini zaidi namna ambavyo amekuwa akifuatilia kaya zile ambazo zimeondolewa. Mpaka sasa tumeshaondoa kaya 63,819 katika maeneo 162 ya utekelezaji.
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, napenda tu
kusema kwamba, wale ambao wamelengwa kuondolewa katika uhakiki huu ni zile kaya ambazo hazikustahili kuingizwa katika mpango. Tumekuwa tukishuhudia pia katika zoezi hili, kama mnavyotambua wakati wa utambuzi na uandikishaji, chombo kikuu kinachoshiriki ni mkutano wetu mkuu wa kijiji au katika shehia lakini unakuta wengine waliwaingiza wenye uwezo matokeo yake baadaye wanajikuta wanakuja kuondolewa tunakuja tunasikia maneno kama hayo.
Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwamba,
kama kweli kaya ilikuwa ni maskini, ikawa imejiboreshea maisha haikutakiwa kuondolewa bila kufuata vigezo vya msingi. Tumeanza kufanya zoezi hili, tumeshawaandikia Wakurugenzi wote tangu mwezi Februari waweze kupitia
kwa kina. Napenda tu kusema kwamba waratibu wengi pia walishiriki, hawakuwa makini katika ufuatiliaji na katika tathmini zao na ndiyo maana tayari tumeshawachukulia hatua waratibu zaidi ya 91 na tutaendelea kufanya hivyo kila ikibidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile napenda tu kusema
kwamba, wale ambao tunawalenga ni wafanyabiashara, unakuta kuna mtu alikuwa ana bucha na mambo mengine ameingizwa, haiwezekani! Vilevile unakuta wengine ni watumishi wa umma wameingizwa katika mpango hawastahili kuanzia siku ya kwanza, hao ndio ambao tunawalenga. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda tu
kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa namna ambavyo wamekuwa wakifuatilia suala hili. Tutaendelea kuwafuatilia na tutaendelea kuchukua hatua. Kwa wale ambao ni maskini kweli kwanza wanatakiwa warudi kwenye mpango na si kumfuatilia aweze kurudisha fedha.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, toka mpango huu umeanza baadhi yetu
tuli-challenge sana kwamba haukuanza kubadilisha fikra za watu kabla ya kuwapa hela. Nataka nimuulize Waziri ni kwa kiwango gani anaweza akaliambia Bunge hili huu mpango
wa kugawa hizi fedha umeleta impact katika jamii, kwa sababu bado hali ya umaskini imeendelea kuwa kubwa katika Taifa letu.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika, naamini, bahati nzuri wiki iliyopita tu tulikuwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, tulikuwa
Iringa Mjini, tumetembelea walengwa wale na kaya zake. Sasa kama leo anasema kaya zile kweli hazijanufaika na hazijaondoka kwenye umaskini, kwa kweli inabidi hata wapiga kura wamwangalie kwa macho mawili, mawili.
(Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa ukiangalia
tumefanya tathmini kuangalia ni kwa namna gani fedha hizi zimeweza kuchochea mabadiliko. Vilevile ukiangalia katika TASAF Awamu ya I na II, kulikuwa hakuna ruzuku ya uhawilishaji lakini ilikuja kuonekana katika Watanzania asilimia 28.3 wenye pengo la umaskini walikuwa hawawezi
kumudu gharama za kupeleka familia zao katika matibabu, wengine watoto wao walikuwa wamedumaa, wengine walikuwa hawapati lishe ya kutosha, wengine walikuwa hata
shuleni mahudhurio hawahudhurii vizuri. Ukiangalia sasa hata Iringa peke yake zaidi ya asilimia 70 mpaka 90 mahudhurio yameimarika, wengine sasa zaidi ya asilimia 10 mpaka 15 wanaanza kukaribia kuondoka katika pengo la umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nipende tu kusema
wengi wameboresha mavazi, wengi ameboresha makazi yao, wengi sasa ukiangalia hata kwa zile kaya zilizokuwa zinajiweza ambazo zilikuwa haziwezi kuwavalisha watoto wao shuleni, wanaangalia kama mtoto maskini anaweza kuvaa nadhifu basi na yeye kidogo anajiongeza. Kwa hiyo, kwa kweli ni Mfuko ambao umekuwa na manufaa sana na nimwombe Mheshimiwa Msigwa aendelee kufuatilia kaya zake na aendelee kuziunga mkono. (Makofi)
MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Spika,
changamoto kubwa ya umaskini Tanzania ni kwamba idadi kubwa ya watu ama wako chini kidogo ya mstari wa umaskini au juu kidogo ya mstari wa umaskini. Kwa hiyo, hata wakipata fedha hizi za TASAF wakipata shock yoyote ya
kimaisha wanarudi chini kwenye mstari wa umaskini na wanakuwa maskini, kwa hiyo, juhudi zote hizi zinakuwa hazijaleta manufaa anayotakiwa. Serikali haioni kwamba umefikia wakati muafaka katika fedha hizi za TASAF kuwe na component ya social protection ili kuhakikisha kwamba baadhi ya watu hawa wanaingizwa kwenye hifadhi ya jamii, wanaweka akiba, wanaweza kupata mikopo midogo midogo ya kuendesha biashara zao, wanaweza wakapata bima ya afya, ili watakapopata shock wasirudi tena kwenye mstari wa umaskini? Haoni kuna haja ya kufanya hivyo sasa hivi kwenye TASAF inayoendelea?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru maana ni hoja ambayo amekuwa akiifuatilia mara kwa mara. Tulipofanya semina katika Bunge hili ambayo iliendeshwa na TASAF pia aliweza kuhoji swali kama hili.
Mheshimiwa Spika, napenda tu kusema kwamba,
lengo la conditional cash transfers kokote duniani ni kuhakikisha kwamba mwisho wa siku ni kuwa na social protection moja ambayo inaunganisha kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Sisi kama TASAF tumeanza na sasa watoto wenye miaka sifuri mpaka tano, mpaka sasa hivi watu wazima
walau kuna hizo component tatu kwenye miradi ya ujira, tunatoa pia ajira za muda, tunatoa miradi ya miundombinu, tuna targeted infrastructure pamoja na mingine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda kusema,tunaiona hoja yake lakini kwa sasa ngoja tumalizie awamu ya kwanza ya awamu ya tatu. Tutakapokuja kusanifu sasa awamu ya pili itakayoanza mwaka 2019/2020 tutaweza kuona ni kwa namna gani swala hili linaweza kuzingatiwa.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza, lakini kabla ya kuuliza swali la nyongeza, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na nimshukuru Mheshimiwa Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniteua kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza ni kuhusu huduma ya TASAF. Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuongeza huduma hii hasa kwa watu wetu maskini kutoka katika Mkoa wetu wa Lindi?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia maendeleo ya jamii, lakini zaidi kwa siku ya kwanza tu ameweza kuuliza swali hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika Mkoa wa Lindi nikitolea tu mfano kwa sasa tuko Lindi DC, Lindi Manispaa, Nachingwea, Ruangwa pamoja na maeneo mengine. Niseme tu kwamba tumepokea hoja hii, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa tumefikia asilimia
70 tumebakiza asilimia 30 yenye vijiji 5,690 na tumepanga katika mwaka huu wa fedha unaokuja wa 2017/2018 tutaweza kutambua na kuandikisha kaya zilizobakia 355,000
na naamini Lindi pia itakuwa ni mojawapo.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniruhusu kuuliza maswali mawili ya
nyongeza.
Mheshimiwa Spika, wakati naandika swali hili, nilitaka lijibiwe na Wizara ya Fedha na si kwamba nilikuwa nimekosea kwa kuitaka Wizara ya Fedha ijibu swali hilo.
Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika na Serikali wanakiri pale ambapo mwekezaji unampunguzia badala
ya kulipa asilimia 25 akalipa asilimia 10 maana yake hiyo ni pesa ambayo ingeweza kwenda kwa Watanzania, ni tax ambayo ilitakiwa kuwa imekusanywa, haikukusanywa.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, isingekuwa busara nafasi hiyo inekuwa imetolewa kwa Mtanzania awae
yeyote ambaye ananunua mabasi ya aina hiyo either anapeleka Mwanza, anapeleka Sumbawanga akaweza
kupata fursa kama hiyo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, katika utaratibu wa Serikali kujenga barabara hizi kwa awamu ya kwanza
ambayo imeshakamilika sasa tunaenda awamu ya pili na mpak aya tatu, ni wazi kwamba Serikali itaendelea kuwekeza na katika hali ya kawaida ili muweze kugawana lazima kila mmoja aoneshe rasilimali ambayo amewekeza. Je, ni busara kwamba pamoja na uwekezaji ambao utaendelea kuwekwa na Serikali, bado mwekezaji huyu aendelee kumiliki asilimia 51 na Serikali ibaki na asilimia 49?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri Mheshimiwa Jafo, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kandege kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tufahamu kwamba mradi huu kwa nature yake ni PPP ni Public Private Partnership na kwa sababu ni PPP na kusema ukweli sisi hatuna uzoefu mkubwa sana wa miradi ya PPP hapa nchini, lakini PPP hii ni PPP ambayo kusema ukweli inagusa the public direct, kwa maana ya usafiri wa wananchi wa Dar es Salaam lakini PPP hii ni PPP ambayo inawahusisha kampuni ya Kitanzania na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la misamaha ni kweli jambo limekuwa likipigiwa kelele kuhusu misamaha.
Ipo misamaha mingi imetolewa na Bunge limekuwa likisema juu ya suala la misamaha. Lakini huu ni msamaha wa aina yake, tena ni kwa eneo ambalo linaleta unafuu kwa wananchi hao hao. Sasa mimi nimuombe tu Mheshimiwa
Kandege aje tumpe details zaidi za suala hili. Pengine swali hili aliliuliza muda mrefu uliopita kwa hiyo limeshabadilika sana na tumekwenda mbali zaidi.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili ameuliza je, katika mwendelezo wa hatua zingine zinazofuata za uendelezaji wa mradi huu, umiliki wa kampuni hii binafsi na Serikali utabakia asilimia ile ile?
Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema tu kwamba katika hiyo asilimia 51 na asilimia 49 ni katika mradi huu wa
awamu hii kwa sababu ni kampuni inayoundwa na Serikali kwa maana ya Simon Group na Serikali wameunda kampuni inayo-operate mabasi haya ya UDART ambayo yanafanya usafiri Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo unaona Serikali katika kila hatua imo na ndiyo maana tusipokuwa makini na jambo
hili sio watu wote wanalipenda na hasa wenzetu. Kwa hiyo, ninaposema wenzetu sina maana upande wowote wa Bunge hapana, nina maana nje kwasababu wangependa PPP ya aina fulani. Nadhani mmenielewa.
Kwa hiyo, niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge, hii ni PPP nzuri ambayo kila kitu kinabaki hapa hapa ingelikuwa
ni kampni imetoka Bogota imetoka wapi, hapo ndio lakini hii ni PPP nzuri na ninaomba sana kama Jiji waliuza hizi asilimia 51 na Serikali tumeweza ku-acquire, kwanza ilikuwa zaidi ya hapo; tumeweza ku-acquire back karibu hizi 49%. Tuendelee lakini ni kwa hatua ya awamu hii tu ndiyo wameshinda hii tender ya kuendesha hii na awamu zinazofuata na zenyewe zitakuwa procured kwa utaratibu mwingine.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa suala la usafiri Jijini Dar
es Salaam hasa public transport ni jambo nyeti na linawagusa wananchi wote kwa ujumla wao; kwa mazoea katika Majiji ya wenzetu Ofisi za Mameya zinahusika sana katika kusimamia usafiri katika Majiji yao. Kwa mfano katika Jiji la London Ofisi ya Meya wa Jiji la London inahusika mpaka kupanga ratiba za treni, ratiba za mabasi na route zenyewe.
Mheshimiwa Spika, nilitaka kujua kwanini katika Jiji la Dar es Salaam Ofisi ya Meya haihusishwi kwa namna yoyote
katika upangaji wa route au kusimamia usafiri katika Jiji la Dae es Salaam?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TA WALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimwa Spika, ni kweli huo ndiyo utaratibu wa Majiji mengi, lakini tatizo letu hapa ni historia ya UDA na Jiji la Dar es Salaam. Jiji la Dar es Salaam waliziuza hizi hisa kwa Kampuni ya Simon Group. Tumejaribu kutafuta namna ya kusaidia, ni Serikali Kuu ndio tuliojitahidi kurudisha asilimia 49 za kwetu maana za zenyewe zilitaka kupotolea huko. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, na kusema ukweli nimpongeze sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika jambo hili
tumeshirikiana vizuri. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa guidance zake mpaka tumeweza hata hizo asilimia 49 zenyewe zilikuwa ni kiini macho. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini Waheshimiwa Wabunge tukumbuke pia historia ya UDA ilivyokuwa, kilikuwa ni kitu
ambacho kimetupwa, kimeachwa huko lakini baadaye kimerudi na kuwa kitu chenye thamani leo ndiyo tunasema.
Waulize wao Jiji la Dar es Salaam wapo, wamewahi kwenda hata Mahakamani kudai kwamba uuzaji huu sio halali? Na kama walikwenda je, ilikuwaje? Na matokeo ya kesi yalikuwaje, mbona sasa hawasemi kwamba tunataka kuappeal?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe sana, Jiji la Dar es Salaam is a legal entity. Wao wanaweza kushtaki na
kushtakiwa, wasije hapa Bungeni, maana walipouziana hawakuleta hapa Bungeni tukapitisha. Waende wakatafute
kama hawakuuza sawasawa waone wanavyoweza kufanya, lakini kwa sasa sisi kama Serikali Kuu tumeweza kurejesha asilimia 49 ya hisa zetu na zinaendeshwa kwenye mikono ya Serikali na tume-win tender ya ku-operate mabasi ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na huyo mwekezaji binafsi.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kabla ya kuuliza swali langu la nyongeza kwa ruhusa yako naomba niweke rekodi
sawasawa, kwamba hisa za Jiji la Dar es Salaam hazikuuzwa jana, ziliuzwa toka mwaka 2009 wakati sisi hatujawa katika uongozi wa Jiji la Dar es Salaam.
Kwa kuwa Waziri ameliambia Bunge kwamba ule mkataba wa uendeshaji wa usafirishaji wa Jiji la Dar es Salaam ni wa muda na kwamba wao Simon Group ndio wameshinda hiyo zabuni, lakini kwa kuwa mkopo uliojenga
miundombinu ya barabara za Jiji za Dar es Salaam umetolewa na Benki ya Dunia, na kwa kuwa mkopo ulionunua magari yaendayo kasi Dar es Salaam umetolewa na Benki ya NMB, na Serikali ndiyo dhamana wa Benki hiyo haoni kwamba sio halali kwa mtu mmoja kumiliki uendeshaji wa mabasi yaendayo kasi Dar es Salaam na kuacha wananchi wengine ambao wana mabasi madogo madogo kuachwa nje ya utaratibu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza NMB ni ya nani? Serikali tuna hisa kwenye NMB. Kwa hiyo hakuna hata dhambi yoyote kwa NMB ku-facilitate, maendeleo ya usafiri wa Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini zile arrangement za NMB na huyu mwekezaji ambaye anaendesha mradi wa mabasi
yaendayo kasi Dar es Salaam ambaye ni Serikali na mwekezaji binafsi it is a PPP, ni mradi ambao una-arrangements zake.
Arrangements zile ni za kati ya UDART ambayo Serikali imo na Simon Group na benki na ujenzi wa miundombinu ni makubaliano ya Serikali na World Bank wala utaratibu wa uendeshaji haukuwa ni jambo muhimu sana, hapa ilikuwa ni kuboresha usafiri katika Jiji la Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, Watanzania wanafahamu adha ya foleni ya Dar es Salaam, Watanzania wanafahamu namna
tunavyopoteza uchumi katika Jiji la Dar es Salaam, hivi kwa nini sisi Watanzani tuna-tend kuchukua PPP. Hatuwezi kujenga hii nchi kwa kutegemea Serikali peke yake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda sana fikra za baadhi ya Wabunge, fikra za kuamini kwamba private sector ni muhimu
katika ujenzi wa uchumi, na siogopi mimi kum-quote Mheshimiwa Zitto Kabwe kwamba ni mtu anayejua sana
eneo hilo la uchumi. Lakini Waziri wa Fedha amekuwa akieleza hapa eneo hilo, lakini bado sisi Watanzania
anaposhiriki mswahili katika shughuli yoyote ya PPP ni nongwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nchi yetu haiwezi kuendelea kwa msingi huu, ila angekuja mgeni kutoka nje angeshangiliwa
kweli kweli, kwani hamjui kwamba kuna hisa nyingi zinachukuliwa kwenye makampuni ambayo Serikali ilitakiwa
kushiriki lakini tumeshindwa.
Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuendelea na msingi huu wa kuendesha uchumi na uchumi ukaenda kama mawazo
yenyewe ndiyo haya.
Mheshimiwa Spika, Serikali inafahamu, imelinda maslahi yake na inafahamu mradi huu umuhimu zaidi si faida
bali huduma kwa wananchi wa Dar es Salaam.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri
ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Ni wazi kwamba Mheshimiwa Waziri amekiri kwamba mfumo huu una upungufu na una changamoto nyingi ambazo nimeelezea mojawapo. Sasa nataka commitment ya Serikali kwamba hiyo Version 11 itaanza kutumika lini? Swali langu la kwanza.
Mheshimiwa Spika, swali la pili; changamoto nyingine ya mfumo huu ni kwamba, unasimama peke yake (stand
alone system) na wakati ukiangalia kwenye taasisi zetu, kwa mfano Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kuna mifumo mingi, tulitegemea kwamba mifumo hii ingekuwa inaongea; kuna EPICA, kuna LGMD, sasa je, Mheshimiwa Waziri atanihakikishia kwamba mfumo huu mpya Lawson Version 11 utakuwa unaongea na mifumo mingine?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nimpongeze sana kwa namna ambavyo amekuwa akisimamia suala zima la management ya rasilimali watu katika utumishi wa umma na yeye mwenyewe pia alikuwa katika utumishi wa umma na tunafahamu mchango wake na tunauthamini.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza, kwamba sasa Toleo hili la 11 ( Lawson Version 11) litaanza lini; nimhakikishie tu kwamba, katika Mwaka huu wa Fedha tumeshatenga Shilingi milioni 486 katika Idara yetu ya
Usimamizi wa Rasilimali Watu pamoja na Idara yetu ya TEHAMA na nimhakikishie tu kwamba katika Mwaka huu wa Fedha suala hili litakamilika. Kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi, tumewakabidhi suala hili Wakala wa Serikali Mtandao ili waweze kusanifu na kusimamia usimikaji wake.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, kwamba ni lini sasa mfumo huu wa usimamizi wa rasilimali watu au
taarifa za kiutumishi na mishahara utaweza kuzungumza na mifumo mingine kama mifumo ya kifedha kama EPICA na mingine; nimwambie tu kwamba tunaiona hoja yake na hata e-government wamekuwa wakifuatilia suala hili kwa makini sana, si tu katika suala zima la kuongea, hata katika kuhakikisha pia gharama za mifumo yenyewe na udurufu wa kuwa na mifumo mingi wakati kunaweza kukawa na mifumo michache ambayo inaweza ikazungumza.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu kwamba pamoja na faida nyingine tutakazozipata tutakapoingia katika
Lawson Version 11 ni pamoja na kuunganisha mifumo mingine kama EPICA lakini pia kuhakikisha Mifumo kama ya NECTA, NIDA, RITA pamoja na mingine nayo pia ni lazima izungumze na Mfumo wetu wa Lawson.
MHE. PETER A. P. LIJUALIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Mimi naomba nifahamu, Jimbo la Kilombero lina Halmashauri mbili, Halmashauri ya Mji wa Ifakara wenye kata tisa na Halmashauri ya Kilombero yenye kata kumi. Kama ambavyo Jimbo la Bariadi ambalo lina Halmashauri mbili, Bariadi Vijijini kuna kata ishirini na moja na Bariadi Mjini kuna kata kumi. Hata hivyo, Mbunge wa Kilombero amezuiliwa na alizuiliwa kushiriki vikao vya Halmashauri ya Kilombero. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipotaka kushiriki nimefungwa miezi sita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwenzangu anashiriki mwanzo mwisho sehemu zote mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nifahamu, ni
kwa nini mimi wa Kilombero siyo tu kwamba nimezuiliwa kushiriki vikao hata kufanya maamuzi kwenye hizi kata zangu kumi sishiriki, lakini mwenzangu wa CCM anashiriki? Sasa naomba Waziri aniambie ni kwa nini ubaguzi huu unafanyika dhidi yangu halafu mwenzangu wa CCM anaachiwa afanye kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nifahamu inawezekana vipi Mbunge wa Kilombero nazuiliwa kushiriki vikao…
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Mheshimiwa Lijualikali ni Mbunge ambaye ana Halmashauri mbili. Kama zilizovyo haki za Wabunge wengine katika majimbo yao na katika Halmashauri zao wanapaswa kuwa wajumbe wa vikao mbalimbali ikiwepo Kamati ya Mipango na Fedha lakini pia na Baraza la Madiwani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inakuwa vigumu sana kulisema jambo hili kwa sababu mhusika angepaswa tu ku-balance interest za maeneo yote na akaweza kufanya Ubunge wake. Kinachotokea ni pale ambapo mhusika pia ni Diwani na Diwani wa upande mmoja wa Jimbo. Kwa hiyo, scenario yake haiwezi ika-fall in all four angles kama ilivyo scenario ya Bariadi. Kwa sababu hiyo Mheshimiwa Mbunge anayo maelekezo yangu ambapo mimi na yeye tulizungumza sana jambo hili tukiwa pamoja na Mheshimiwa Kiwanga ambayo hayo hayatekelezi. Hivyo, kwa sababu ameleta jambo hili hapa Mheshimiwa Lijualikali ofisi yangu ipo, njoo tuzungumze tuone huo ugumu unaoupata na kwa nini haitokei hivyo, tutalimaliza jambo hili, nakukaribisha sana ofisini.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba niulize swali kwamba mwaka 2013 Mji Mdogo wa Igunga ulianzishwa na tumekuwa na tatizo hili ambalo wanalisema wote kwamba umeanzishwa lakini haufanyi kazi. Namshukuru Waziri ameeleza kwenye swali namba 142 kwamba ni Halmashauri inatakiwa isimamie, lakini sisi tumejaribu kuishauri Halmashauri isimamie jambo hilo na nimeweza kufika ofisini kwake mara moja na akaahidi kwamba angeweza kuandika Waraka wa kumwambia Mkurugenzi au kuiambia Halmashauri ifanye jambo hilo na halijafanyika.
Namuomba Mheshimiwa Waziri hebu utusaidie kwa sababu DED sasa hivi hataki kabisa kuisikiliza hiyo Mamlaka ya Mji Mdogo wa Igunga na hawana bajeti, hawana gari, wana mtendaji tu. Tunaomba Mheshimiwa Waziri utusaidie kama ikiwezekana njoo Igunga ili mamlaka hii iweze kuanza. Ahsante sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia swali la Mheshimiwa Mbunge na tutawasiliana tuone namna bora ya kulifanya jambo hili kwa sababu ni kweli tumekwishazungumza na ni kweli nilikwishatoa maagizo lakini halitekelezeki. Kama nilivyosema, mamlaka hizi zinapoanzishwa zinalelewa na Halmashauri Mama. Kwa hiyo, kama hakuna mipango madhubuti inayopanga mchakato wa namna ya kutafuta rasilimali fedha na rasilimali watu basi tatizo linakuwa kubwa zaidi. Kwa hiyo, tutajaribu kuliona namna lilivyo na halina tofauti sana na scenario za Miji mingine Midogo iliyoanzishwa ili tuone namna bora ya kuweza kulifanya.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana katika Halmashauri mbalimbali nchini baada ya kauli ya Mheshimiwa Rais katika sherehe za Mei Mosi juzi kule Kilimanjaro alivyosema kwamba Halmashauri yoyote au Baraza lolote la Madiwani litakalojitokeza na kutaka kumuondoa Mkurugenzi kazini au kumfukuza, Baraza hilo litavunjwa mara moja na yeye ndiye mwenye mamlaka ya kumteua Mkurugenzi kwa hiyo atahakikisha anaifuta Halmashauri hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa mujibu wa Sheria
za Serikali za Mitaa, Waheshimiwa Madiwani ndiyo wasimamizi wa shughuli na miradi ya maendeleo na mapato na matumizi ya fedha za Halmashauri.
Je, Mkurugenzi akiwa ametumia fedha vibaya na akatumia madaraka yake vibaya, ni utaratibu gani ambao Waheshimiwa Madiwani watautumia kama siyo kumuondoa Mkurugenzi wakati Rais tayari ameshawaonya na amewaambia kwamba ataivunja Halmashauri hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza si kweli kwamba kauli ya Mheshimiwa Rais imeleta mkanganyiko. Kauli ya Mheshimiwa Rais imemaanisha pale ambapo mkakati unafanywa na Waheshimiwa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi kwa maslahi binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uzoefu wa mwaka wangu mmoja na miezi kadhaa yote mawili yanatokea, wakati mwingine kunakuwa na mkakati wa upande wa watumishi kumuondoa Mwenyekiti na wakati mwingine kuna mkakati kwa upande wa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi kwa sababu tu maslahi yamegongana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais anapolizungumzia hili hazungumzii kwa scenario unayoisema ya kwamba kumetokea ubadhirifu na wala Mheshimiwa Rais halindi wabadhirifu, anazungumzia pale ambapo kuna utaratibu unapangwa wa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi anayesimamia watu wasifanye wizi, ndicho anachokizungumzia.
Kwa hiyo, huo mfano mwingine baki nao lakini wa
Rais ni huu aliokuwa anausema kwamba pale kunapokuwa kuna mkakati wa kumuondoa Mkurugenzi ambaye anasimamia fedha za Halmashauri hapo yuko tayari kuivunja Halmashauri na mimi mwenyewe nasema wala haitafika hata kwake mimi mwenyewe nitavunja hiyo Halmashauri.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza Mbunge aliyeuliza swali kwamba Wabunge wanatumia zile pesa, namshukuru sana Naibu Waziri alivyoeleza kuhusu zile pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa Wabunge hawashiki, pesa zinakwenda kwa Mkurugenzi, Mwenyekiti yeye ni Mwenyekiti tu. Kuna Afisa Mipango, kuna Madiwani wawili, kuna watendaji wawili ndipo utagawa zile pesa, hatugusi hata senti tano moja sisi kuweka kwenye mafuta.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mfuko wa Jimbo nimezungumza tangu mara ya kwanza una matatizo. Kuna majimbo mengine na tujimbo twingine.
Huu mfuko hauwezi kufutwa kwa sababu kuna Wabunge wengine kama Viti Maalum, mzee wangu anasema Majimbo, Majimbo mengine yana watu 30, watu 40, mengine kata 10 Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kama nilivyosema mara ya kwanza usimamishwe, wafanye tathmini upya, wagawe upya kutokana na idadi ya watu na ukubwa wa majimbo. Haiwezekani kuna majimbo mengine ni madogo wanapewa sawa na Jimbo kubwa haiwezekani. Ifanywe tathmini upya ili hela ziende kwa usawa bila ubaguzi wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majimbo ambayo hayana vigezo, hayastahili kuapata mfuko wa Jimbo mkubwa, haiwezekani. Jimbo lako la Ilala kubwa lipate sawa na Jimbo...
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuende na takwimu sahihi, haiwezekani.
Swali, Wabunge Viti Maalum hawaruhusiwi kupata Mfuko wa Jimbo na wasitegemee kuzipata, kwa sababu Mbunge wa Jimbo ndiyo anastahili kupata ule Mfuko wa Jimbo na ikiwezekana Wabunge wale wengine wachunguzwe walikotoka. Haiwezekani wewe uliyekuja kuzungumza hapa wakati ulikotoka wewe hauna hata wa...(Kicheko)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Keissy ameuliza maswali ya nyongeza pia ametoa maelezo ya nyongeza. Hata hivyo katika maelezo yake kuna vitu vya msingi amevisema.
Kwanza ambacho ndicho nitakachokijibu vingine nitaviacha kwa sababu kwa mujibu wa Kanuni natakiwa kujibu swali moja. Ni kweli kwamba kuna vigezo vinavyotumika katika kugawa fedha hizi, vigezo hivi vimesemwa katika jibu la msingi. Kigezo cha kwanza ni idadi ya watu ambayo ni asilimia 45. Mgao sawa kwa kila Jimbo asilimia 25, kiwango cha umaskini asilimia 20, ukubwa wa eneo asilimia 10. Fedha yoyote itakayotengwa kwenye bajeti hapa itaingizwa katika hii formula.
Kwa hiyo, bahati mbaya sana kwa mwaka huu wa fedha, fedha iliyotengwa ilikua kidogo kwa sababu Hazina hawakutambua majimbo haya mapya, hatukuwa na mawasiliano mazuri. Nataka niwahakikishie kwamba kigezo hiki sasa kwa mwaka huu wa fedha tumesahihisha hayo makosa yote na sasa majimbo yote yanahesabika, yaliyoongezeka na kosa hilo halitafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kuna baadhi ya Majimbo yanapewa fedha kidogo kwa mujibu wa formula hii, hilo haliwezekani isipokuwa fedha zimeshuka tu kwa sababu zilikuwa kidogo na tulilazimika kuziingiza kwenye formula hii kama zilivyo, ndiyo maana ni tofauti na iliyotolewa nyuma na iliyotolewa sasa.
MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naitwa Mmasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu nimkumbushe Kaka yangu Jafo. Kaka yangu Mheshimiwa Naibu Waziri tulipokuja hapa Bungeni mimi na wewe tulikula kiapo kimoja, tofauti yetu ilikuwa kwenye majina. Mimi nilitamka Ester Michael Mmasi na wewe ukatamka jina lako kadri ilivyo kwenye kumbukumbu za Bunge hili. Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye maslahi ya Kibunge hususani katika payroll ya Bunge sote tuna maslahi sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu hapa yametoka kwamba hawa wenzetu kupitia Mfuko wa Jimbo wanafanya kazi za wananchi, sisi ni akina nani na tunafanya kazi za nani?Hatufanyi kazi za familia zetu, tunafanya kazi za wananchi hawa hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia nchi ya Kenya, mathalani Wabunge...
MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Wabunge wa Kenya hili linafanyika. Nenda tukaangalie Wabunge wa Kenya (Woman MP’s) kwenye county level wana-Capital Development Funds for women MP’s, kwa nini Tanzania ishindikane?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa naomba kujibu swali ambalo nadhani litakuwa swali maarufu la mwaka na limeulizwa kwa staili ambayo haijawahi kufanyika, ninakupongeza Mwenyekiti kwa utaalamu wa kujua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linahusu Mfuko wa Jimbo na Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Ester Mmasi, Mheshimiwa Munde Abdallah na wengine wengi Wabunge wa Viti Maalum wanataka na wao wapate mgao wa fedha za Mfuko wa Jimbo. Swali hili siyo kwamba linaulizwa kwa mara ya mwanzo leo, limekuwa likiulizwa na mara nyingi tumekuwa tukitoa majawabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu maarufu ambayo tumeyatoa kwamba tutakwenda kushughulikia tuone utaratibu wake, lakini kila tunaposhughulikia tunapata ugumu kwa sababu mfuko huu umezaliwa kwa mujibu wa sheria, sheria yenyewe inaitekeleza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mfuko wenyewe unaitwa Mfuko wa Jimbo na kwa hiyo, kuupa jina linguine lolote lile ni kazi ngumu kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani kuna Wabunge
wa Majimbo, kuna Wabunge wa Viti Maalum, kuna Wabunge wa Mikoa, kuna Wabunge wanaoteuliwa na Mheshimiwa Rais. Bunge hili likitambua kwamba Wabunge wa aina hizi zote wapo, lilitunga Sheria ya Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye instrument yangu kwa mujibu wa sheria nilizopewa kuzisimamia nina sheria inayosema nitasimamia Mfuko wa Jimbo, haisemi vinginevyo. Ndiyo maana kwenye jibu letu la msingi nimesema kama Bunge litaona vinginevyo suala hilo linakuja kwa utaratibu mwingine, lakini kwa sasa mimi ninasimamia Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale Wabunge waliokuwa wanadai sana mfuko huu, waliokuwa wa Viti Maalum, walipopata majimbo na wenyewe msimamo wao umebadilika, ni kwa sababu ya majukumu anayoyapata Mbunge wa Jimbo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mengine yameulizwa na Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim ambaye ameuliza suala la fedha kuchelewa Zanzibar, hili tumelichukua, tunawasiliana na Ofisi ya Makamu wa Rais tuone utaratibu bora zaidi wa kuweza kufanya fedha hizo ziwafikie Wabunge wa Zanzibar, hasa tunatambua yapo mapendekezo ya kwamba bora zikapita katika Ofisi ya Bunge Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine dogo limeulizwa na Mheshimiwa Paresso kwamba Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye Kamati za Fedha. Kamati za Fedha zinatambua uwepo wa Madiwani na Mbunge unapoingia kwenye Halmashauri huwi Mbunge unakuwa Diwani, kule kwenye Kamati ya Fedha wanaoteuliwa kuingia kwenye Kamati ya Fedha huwa ni Madiwani. Sasa nadhani ni utaratibu wa Halmashauri zenu, kama wewe Mbunge kuteuliwa kuna baadhi ya Wabunge ambao wanaingia kwenye Kamati ya Fedha, lakini kule wameingia kwa tiketi ya Udiwani wao kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napata shida hapa
kwa sababu la kwanza, kwamba kwa Majimbo ambayo yana Wabunge wengi wa Viti Maalum, na mfahamu kikao kile kina utaratibu wa gharama zake na mambo mengine. Ingawa gharama siyo hoja kubwa, lakini kwa Jimbo ambalo lina Wabunge wa Viti Maalum nane, 10, sijui hali itakuwaje kwa sababu gharama za uendeshaji wa Halmashauri zitakuwa kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ingelikuwa Wabunge labda ni mmoja au wawili pengine unaweza kuichukulia hili jambo likawezekana, lakini kwa hali ilivyo kuna tatizo kubwa sana na ninadhani ni vema hili jambo likabaki kama ilivyo na ndio utaratibu ulivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tiketi ya Udiwani, Mbunge anaweza akateuliwa na Mwenyekiti kwa utaratibu ule akawa Mjumbe wa Kamati ya Fedha.(Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.
Ubaguzi huu wa Wabunge kati ya Wabunge wa Viti Maalum na Wabunge wa Majimbo pamoja na kutokupewa Mifuko ya Jimbo, lakini pia hatuingii katika Kamati za Fedha kwenye Halmashauri zetu na jambo hili tumeshalisema muda mrefu, kwa nini Serikali inakuwa na kigugumizi kuruhusu Wabunge wa Viti Maalum katika Halmashauri tulizowapa tusiingie katika Kamati ya Fedha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge wa Viti Maalum ni hofu tu, tutawang’oa Majimboni. (Makofi/Kicheko)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa naomba kujibu swali ambalo nadhani litakuwa swali maarufu la mwaka na limeulizwa kwa staili ambayo haijawahi kufanyika, ninakupongeza Mwenyekiti kwa utaalamu wa kujua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linahusu Mfuko wa Jimbo na Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Ester Mmasi, Mheshimiwa Munde Abdallah na wengine wengi Wabunge wa Viti Maalum wanataka na wao wapate mgao wa fedha za Mfuko wa Jimbo. Swali hili siyo kwamba linaulizwa kwa mara ya mwanzo leo, limekuwa likiulizwa na mara nyingi tumekuwa tukitoa majawabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu maarufu ambayo tumeyatoa kwamba tutakwenda kushughulikia tuone utaratibu wake, lakini kila tunaposhughulikia tunapata ugumu kwa sababu mfuko huu umezaliwa kwa mujibu wa sheria, sheria yenyewe inaitekeleza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mfuko wenyewe unaitwa Mfuko wa Jimbo na kwa hiyo, kuupa jina linguine lolote lile ni kazi ngumu kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani kuna Wabunge
wa Majimbo, kuna Wabunge wa Viti Maalum, kuna Wabunge wa Mikoa, kuna Wabunge wanaoteuliwa na Mheshimiwa Rais. Bunge hili likitambua kwamba Wabunge wa aina hizi zote wapo, lilitunga Sheria ya Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye instrument yangu kwa mujibu wa sheria nilizopewa kuzisimamia nina sheria inayosema nitasimamia Mfuko wa Jimbo, haisemi vinginevyo. Ndiyo maana kwenye jibu letu la msingi nimesema kama Bunge litaona vinginevyo suala hilo linakuja kwa utaratibu mwingine, lakini kwa sasa mimi ninasimamia Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale Wabunge waliokuwa wanadai sana mfuko huu, waliokuwa wa Viti Maalum, walipopata majimbo na wenyewe msimamo wao umebadilika, ni kwa sababu ya majukumu anayoyapata Mbunge wa Jimbo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mengine yameulizwa na Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim ambaye ameuliza suala la fedha kuchelewa Zanzibar, hili tumelichukua, tunawasiliana na Ofisi ya Makamu wa Rais tuone utaratibu bora zaidi wa kuweza kufanya fedha hizo ziwafikie Wabunge wa Zanzibar, hasa tunatambua yapo mapendekezo ya kwamba bora zikapita katika Ofisi ya Bunge Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine dogo limeulizwa na Mheshimiwa Paresso kwamba Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye Kamati za Fedha. Kamati za Fedha zinatambua uwepo wa Madiwani na Mbunge unapoingia kwenye Halmashauri huwi Mbunge unakuwa Diwani, kule kwenye Kamati ya Fedha wanaoteuliwa kuingia kwenye Kamati ya Fedha huwa ni Madiwani. Sasa nadhani ni utaratibu wa Halmashauri zenu, kama wewe Mbunge kuteuliwa kuna baadhi ya Wabunge ambao wanaingia kwenye Kamati ya Fedha, lakini kule wameingia kwa tiketi ya Udiwani wao kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napata shida hapa
kwa sababu la kwanza, kwamba kwa Majimbo ambayo yana Wabunge wengi wa Viti Maalum, na mfahamu kikao kile kina utaratibu wa gharama zake na mambo mengine. Ingawa gharama siyo hoja kubwa, lakini kwa Jimbo ambalo lina Wabunge wa Viti Maalum nane, 10, sijui hali itakuwaje kwa sababu gharama za uendeshaji wa Halmashauri zitakuwa kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ingelikuwa Wabunge labda ni mmoja au wawili pengine unaweza kuichukulia hili jambo likawezekana, lakini kwa hali ilivyo kuna tatizo kubwa sana na ninadhani ni vema hili jambo likabaki kama ilivyo na ndio utaratibu ulivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tiketi ya Udiwani, Mbunge anaweza akateuliwa na Mwenyekiti kwa utaratibu ule akawa Mjumbe wa Kamati ya Fedha.(Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ningependa nimuulize Mheshimiwa Waziri swali lifuatalo:-
Kwa kuwa fedha za Mfuko wa Jimbo pale ambapo zinaingizwa kwenye akaunti kwa upande wa Tanzania Bara, kwa upande wa Zanzibar zinachukua karibu miezi minne mpaka mitano kutokana na mlolongo mrefu ambapo fedha hizi zinaingizwa katika akaunti zetu za Majimbo ndani ya Wabunge wa Visiwa vya Unguja na Pemba.
Ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, ni sababu zipi za msingi zinazopelekea fedha zinapoingia katika akaunti za Majimbo ya Tanznaia Bara zinachukua miezi sita kwa upande wa Tanzania Zanzibar. Je, nini kifanyike ili fedha hizi ziweze kufika kwa wakati kama ambavyo zinavyoingia upande huu? Nashukuru sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa naomba kujibu swali ambalo nadhani litakuwa swali maarufu la mwaka na limeulizwa kwa staili ambayo haijawahi kufanyika, ninakupongeza Mwenyekiti kwa utaalamu wa kujua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linahusu Mfuko wa Jimbo na Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Ester Mmasi, Mheshimiwa Munde Abdallah na wengine wengi Wabunge wa Viti Maalum wanataka na wao wapate mgao wa fedha za Mfuko wa Jimbo. Swali hili siyo kwamba linaulizwa kwa mara ya mwanzo leo, limekuwa likiulizwa na mara nyingi tumekuwa tukitoa majawabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu maarufu ambayo tumeyatoa kwamba tutakwenda kushughulikia tuone utaratibu wake, lakini kila tunaposhughulikia tunapata ugumu kwa sababu mfuko huu umezaliwa kwa mujibu wa sheria, sheria yenyewe inaitekeleza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mfuko wenyewe unaitwa Mfuko wa Jimbo na kwa hiyo, kuupa jina linguine lolote lile ni kazi ngumu kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani kuna Wabunge
wa Majimbo, kuna Wabunge wa Viti Maalum, kuna Wabunge wa Mikoa, kuna Wabunge wanaoteuliwa na Mheshimiwa Rais. Bunge hili likitambua kwamba Wabunge wa aina hizi zote wapo, lilitunga Sheria ya Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye instrument yangu kwa mujibu wa sheria nilizopewa kuzisimamia nina sheria inayosema nitasimamia Mfuko wa Jimbo, haisemi vinginevyo. Ndiyo maana kwenye jibu letu la msingi nimesema kama Bunge litaona vinginevyo suala hilo linakuja kwa utaratibu mwingine, lakini kwa sasa mimi ninasimamia Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale Wabunge waliokuwa wanadai sana mfuko huu, waliokuwa wa Viti Maalum, walipopata majimbo na wenyewe msimamo wao umebadilika, ni kwa sababu ya majukumu anayoyapata Mbunge wa Jimbo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mengine yameulizwa na Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim ambaye ameuliza suala la fedha kuchelewa Zanzibar, hili tumelichukua, tunawasiliana na Ofisi ya Makamu wa Rais tuone utaratibu bora zaidi wa kuweza kufanya fedha hizo ziwafikie Wabunge wa Zanzibar, hasa tunatambua yapo mapendekezo ya kwamba bora zikapita katika Ofisi ya Bunge Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine dogo limeulizwa na Mheshimiwa Paresso kwamba Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye Kamati za Fedha. Kamati za Fedha zinatambua uwepo wa Madiwani na Mbunge unapoingia kwenye Halmashauri huwi Mbunge unakuwa Diwani, kule kwenye Kamati ya Fedha wanaoteuliwa kuingia kwenye Kamati ya Fedha huwa ni Madiwani. Sasa nadhani ni utaratibu wa Halmashauri zenu, kama wewe Mbunge kuteuliwa kuna baadhi ya Wabunge ambao wanaingia kwenye Kamati ya Fedha, lakini kule wameingia kwa tiketi ya Udiwani wao kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napata shida hapa
kwa sababu la kwanza, kwamba kwa Majimbo ambayo yana Wabunge wengi wa Viti Maalum, na mfahamu kikao kile kina utaratibu wa gharama zake na mambo mengine. Ingawa gharama siyo hoja kubwa, lakini kwa Jimbo ambalo lina Wabunge wa Viti Maalum nane, 10, sijui hali itakuwaje kwa sababu gharama za uendeshaji wa Halmashauri zitakuwa kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ingelikuwa Wabunge labda ni mmoja au wawili pengine unaweza kuichukulia hili jambo likawezekana, lakini kwa hali ilivyo kuna tatizo kubwa sana na ninadhani ni vema hili jambo likabaki kama ilivyo na ndio utaratibu ulivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tiketi ya Udiwani, Mbunge anaweza akateuliwa na Mwenyekiti kwa utaratibu ule akawa Mjumbe wa Kamati ya Fedha.(Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuuliza swali.
Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba pesa zile za Jimbo huwa zinakwenda kutumika kwa wananchi; na kwa kuwa Wabunge wa Viti Maalum wanafanya kazi na wananchi hao hao; na kwa kuwa tumelisema suala hili kuanzia mwaka 2011 mpaka leo hii na Serikali bado ina kigugumizi, bado inaona ugumu kuwapa pesa Wabunge wa Viti Maalum, huenda bajeti ya Serikali haiko vizuri.
Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari sasa kwa nia njema kabisa ya kusaidia Wabunge hawa wa Viti Maalum, walau kila Mbunge wa Jimbo husika kwa mfano kwangu mimi nina Majimbo 11, kila Mbunge wa Jimbo husika walau akakatwa asilimia 10 ya Mfuko wa Jimbo ikakaa kwa Mkurugenzi, amount ya pesa zile wakagaiwa Wabunge wa Majimbo siyo kugaiwa cash, zikakaa kwa Mkurugenzi labla mimi nikawa na milioni nne tu, nikaenda eneo fulani nikakuta hamna gloves nikawaambia zile milioni nne Mkurugenzi m-deposit kwa ajili ya kina mama? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa naomba kujibu swali ambalo nadhani litakuwa swali maarufu la mwaka na limeulizwa kwa staili ambayo haijawahi kufanyika, ninakupongeza Mwenyekiti kwa utaalamu wa kujua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linahusu Mfuko wa Jimbo na Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Ester Mmasi, Mheshimiwa Munde Abdallah na wengine wengi Wabunge wa Viti Maalum wanataka na wao wapate mgao wa fedha za Mfuko wa Jimbo. Swali hili siyo kwamba linaulizwa kwa mara ya mwanzo leo, limekuwa likiulizwa na mara nyingi tumekuwa tukitoa majawabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu maarufu ambayo tumeyatoa kwamba tutakwenda kushughulikia tuone utaratibu wake, lakini kila tunaposhughulikia tunapata ugumu kwa sababu mfuko huu umezaliwa kwa mujibu wa sheria, sheria yenyewe inaitekeleza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mfuko wenyewe unaitwa Mfuko wa Jimbo na kwa hiyo, kuupa jina linguine lolote lile ni kazi ngumu kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani kuna Wabunge
wa Majimbo, kuna Wabunge wa Viti Maalum, kuna Wabunge wa Mikoa, kuna Wabunge wanaoteuliwa na Mheshimiwa Rais. Bunge hili likitambua kwamba Wabunge wa aina hizi zote wapo, lilitunga Sheria ya Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye instrument yangu kwa mujibu wa sheria nilizopewa kuzisimamia nina sheria inayosema nitasimamia Mfuko wa Jimbo, haisemi vinginevyo. Ndiyo maana kwenye jibu letu la msingi nimesema kama Bunge litaona vinginevyo suala hilo linakuja kwa utaratibu mwingine, lakini kwa sasa mimi ninasimamia Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale Wabunge waliokuwa wanadai sana mfuko huu, waliokuwa wa Viti Maalum, walipopata majimbo na wenyewe msimamo wao umebadilika, ni kwa sababu ya majukumu anayoyapata Mbunge wa Jimbo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mengine yameulizwa na Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim ambaye ameuliza suala la fedha kuchelewa Zanzibar, hili tumelichukua, tunawasiliana na Ofisi ya Makamu wa Rais tuone utaratibu bora zaidi wa kuweza kufanya fedha hizo ziwafikie Wabunge wa Zanzibar, hasa tunatambua yapo mapendekezo ya kwamba bora zikapita katika Ofisi ya Bunge Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine dogo limeulizwa na Mheshimiwa Paresso kwamba Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye Kamati za Fedha. Kamati za Fedha zinatambua uwepo wa Madiwani na Mbunge unapoingia kwenye Halmashauri huwi Mbunge unakuwa Diwani, kule kwenye Kamati ya Fedha wanaoteuliwa kuingia kwenye Kamati ya Fedha huwa ni Madiwani. Sasa nadhani ni utaratibu wa Halmashauri zenu, kama wewe Mbunge kuteuliwa kuna baadhi ya Wabunge ambao wanaingia kwenye Kamati ya Fedha, lakini kule wameingia kwa tiketi ya Udiwani wao kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napata shida hapa
kwa sababu la kwanza, kwamba kwa Majimbo ambayo yana Wabunge wengi wa Viti Maalum, na mfahamu kikao kile kina utaratibu wa gharama zake na mambo mengine. Ingawa gharama siyo hoja kubwa, lakini kwa Jimbo ambalo lina Wabunge wa Viti Maalum nane, 10, sijui hali itakuwaje kwa sababu gharama za uendeshaji wa Halmashauri zitakuwa kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ingelikuwa Wabunge labda ni mmoja au wawili pengine unaweza kuichukulia hili jambo likawezekana, lakini kwa hali ilivyo kuna tatizo kubwa sana na ninadhani ni vema hili jambo likabaki kama ilivyo na ndio utaratibu ulivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tiketi ya Udiwani, Mbunge anaweza akateuliwa na Mwenyekiti kwa utaratibu ule akawa Mjumbe wa Kamati ya Fedha.(Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa matatizo makubwa yanayowakabili watu wenye ulemavu hasa waishio vijijini ni umaskini uliokithiri kwa jamii hii. Mbali ya Serikali kutoa maagizo kwa
Halmashauri kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri.
Je, Serikali sasa ina mkakati gani kuhakikisha kwamba inapunguza umaskini kwa kundi hili la watu wenye ulemavu ambalo liko nyuma?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, sababu kubwa kama nilivyoeleza inayopelekea watu wenye ulemavu kuwa na maisha duni ni pamoja na kutozingatiwa kwa mahitaji yao wanayoyapendekeza katika ngazi mbalimbali wakati wa bajeti.
Pamoja na hizo sababu mambo hayo yanapuuzwa, kwa kuwa bajeti ya Serikali bado kusomwa; je, Serikali haioni muhimu sasa wa kuangalia uwezekano wa kutenga fedha kwa Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu ambao katika bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu haukutengewa hata shilingi, sasa tuangalie ni kwa jinsi gani
basi tutatenga fedha ili tuweze kusaidia kundi hili? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Sheria Namba 9 ya mwaka 2010 inazitaka Mamlaka za Mikoa kusimamia uanzishaji wa Kamati za Walemavu kwenye Mikoa, Halmashauri, Kata na Vijiji na tulishaagiza kama alivyosema kwenye jibu la msingi Naibu Waziri Mheshimiwa Mavunde, lakini nichukue nafasi hii sasa kutaka nitoe agizo kwa Wakuu wa Mikoa wote kuhakikisha kwamba Kamati hizi sasa tuwape deadline ndani ya miezi mitatu kuanzia siku ya leo ziundwe hizi Kamati, Wakuu wa Mikoa wahakikishe Kamati hizi zinaundwa katika Mikoa, Halmashauri, Kata na Vijiji na zaidi ya hapo tutachukua hatua kwa sababu maagizo mengine kama haya yana umuhimu mkubwa kwa sababu yanazaa tena mafanikio mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Mbunge hapa anauliza katika bajeti hajaona kitu chochote kilichotengwa kwa ajili ya ulemavu, pamoja na kwamba sekta mbalimbali zinashughulika na jambo la walemavu na kwamba suala la ulemavu ni suala mtambuka, lakini sisi kama Mamlaka ya Serikali za Mitaa tunatafakari maombi makubwa yaliyoletwa wakati wa mjadala wa bajeti ya Wizara yangu ambapo maoni mengi ikiongozwa na Mheshimiwa Ikupa alisema wanaomba basi angalau asilimia mbili ya own source ya makusanyo ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa iwekwe kwa ajili ya Walemavu na hili ni jambo ambalo tumeliafiki kwa hatua za awali, lakini tutaendelea kulitafakari kuona namna
gani tunalitekeleza. Sasa inawezekana pia likatekelezwa vizuri endapo Kamati hizi sasa zitaundwa katika level hizi zote za Mkoa, Wilaya, Kata, Halmashauri na Vijiji. Zikiwepo hizi Kamati ndiyo rahisi kutekeleza hata huo mgawanyo wa hiyo asilimia mbili ya makusanyo ya ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, nikubaliane kabisa kwamba Serikali tuko tayari na tutahakikisha kwamba tunalisimamia jambo hili vizuri kabisa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Simbachawene kwa jibu la nyongeza namba moja lililokuwa linahusu Kamati kwa mujibu wa Sheria Namba 9 ya mwaka 2010 ya Huduma za Walemavu nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongeze majibu ya ziada kwa swali la nyongeza namba mbili linalohusu Mfuko wa Walemavu ambao nao unazingatia Sheria Namba 9 ya mwaka 2010.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa anasoma bajeti yake na kuhitimisha hoja yake hapa ndani, alilieleza Bunge lako Tukufu kupitia utaratibu ambao tumejiwekea wa Vikao vya Baraza la Watu Wenye Ulemavu ambalo sasa limeanza kufanya kazi. Tumeanza pia kufanya kazi ya kufanya mapitio ya kuona ni namna gani Serikali inaweza kushughulikia pia mfuko huo wa watu wenye ulemavu, vilevile kushirikiana na nguvu hizo nyingine ambazo zimesemwa mbele ya Bunge lako Tukufu
ambazo zinaweza zikasaidia watu wenye elemavu wakapata fursa sawa na watu wengine wote katika nchi yetu ya Tanzania, kupitia mifuko mbalimbali ambayo imeanzishwa na mingi ikiwa inasimamiwa na Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kuwa suala hili linafanyiwa kazi kwa kina sana na linaratibiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu ndani ya ofisi yake na tutaendelea kulifanyia kazi ya kutosha. (Makofi)
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mimi swali langu dogo tu, nilikuwa naomba, maana uzoefu inaonekana kama Waziri Mkuu ama Waziri wa TAMISEMI anafika katika eneo kuangalia hali halisi ya matatizo ndiyo pale inapomuuma katika moyo na kutoa kipaumbele katika haya maeneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba ni lini sasa Waziri wa TAMISEMI ama Waziri Mkuu atafika kwenye Jimbo la Mlimba ili aangalie matatizo alie na machozi halafu aone sympathy ya kuwasaidia wananchi wa Mlimba katika masuala ya magari, afya na mambo mengine? Ni hapa tu.(Makofi/Kicheko)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kiwanga kwamba tulifanya ziara ofisi yetu, tumetembelea Halmashauri zote kati ya Halmashauri 185 tumebakisha chini ya Halmashauri kumi hivi sasa na moja ikiwa yako ya Mlimba. Ndiyo maana tumekubaliana hapa na nimezungumza katika kipindi mbalimbali kwamba baada ya Bunge nitakuwa na session maalum katika Mkoa wa Morogoro kumalizia Halmashauri zilizobaki na Mkoa wa Songwe, vilevile nitaenda kule Ukerewe pamoja na Mara ambako kuna Rorya, Tarime na Serengeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, hayo tunaenda kuyafanya lengo kubwa ni kufikia maeneo mbalimbali tubadilishane mawazo tikiwa site kule tukubaliane, tubaini changamoto halafu tujadiliane, nini tutafanya ili kuwahudumia wananchi. Kwa hiyo, naomba nikutoe hofu katika hilo tutaenda kulifanya katika kipindi cha sasa.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu kuhusiana na ujenzi wa kituo cha mabasi ya Kusini katika eneo la Jimbo la Mkuranga; na kwa kuwa uratibu wa zoezi zima la ujenzi wa kituo cha mabasi ya Kusini linasimamiwa pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kuhakikisha wanashirikiana vema, Wizara ya TAMISEMI, Maliasili na nyingine zinazohusika kuhakikisha kituo hiki cha mabasi ya Kusini kinapatikana kwa haraka katika eneo la Wilaya ya Mkuranga hasa maeneo ya msitu ule wa Vikindu? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ujenzi wa vituo hivi vya mabasi ni uwekezaji mkubwa sana na ni vyanzo vikubwa vya mapato kwenye Halmashauri zetu. Ukizingatia Sheria ya Fedha ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, huwezi kwa namna yoyote ile ukafanya mradi kwenye mamlaka ya Serikali ya Mtaa husika na mradi ule ukawa na wadau wengi nje ya utaratibu wa kuibua na kutekeleza mradi ule kutoka kwenye Halmashauri husika.
Kwa hiyo, kwa kuzingatia dhana ya ugatuaji wa madaraka (D by D), katika kusimamia sisi kama TAMISEMI tutajaribu sana kuhakikisha kwamba miradi hii ya vituo vya mabasi itafanywa na mamlaka za Serikali za Mitaa husika kwa kushirikiana na wadau wowote whether ni PPP au kwa kushirikiana na taasisi zetu za Mifuko ya Jamii, kwa vyovyote vile lakini mwenye mradi na mmiliki wa mradi atakuwa ni Halmashauri husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kumueleza kwamba sisi kama Serikali kwa kushirikiana na TAMISEMI na Wizara ya Maliasili tutakuwa tu ni facilitator lakini pia kuwaondolea vikwazo ili waweze kutekeleza mradi huo. Hii naisema ni kwa maeneo yote, kwa Mbezi Luis lakini pia kwa Boko, utaratibu utakuwa ni huo huo.(Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Pamoja na upungufu huu, kuna tatizo kubwa sana la mgawanyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua, ni kwa nini Wizara ya TAMISEMI inapanga moja kwa moja badala ya kuhakikisha kwamba Halmashauri ndiyo zinakuwa na huo utaratibu kwa sababu wao ndio wanajua upungufu wa Walimu? Kwa hiyo, nataka kujua na kazi za Maafisa Elimu sasa itakuwa nini?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kama ni wa sekta ya afya, basi Wizara ya Afya inaweza ikatoa tangazo na ikawaingiza kwenye ajira ya Serikali na baadaye taratibu nyingine za kiutumishi kufanywa na Wizara ya Utumishi na baadaye wale watumishi wanakabidhiwa TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma kulitokea matatizo kwamba tukiwapeleka huko hawafiki na ndiyo maana sisi TAMISEMI tukaamua kuwapangia mpaka na vituo vyao, lakini hatufanyi hivyo bila consultation na mamlaka husika, wanakuwa wanatuambia upungufu uko wapi na wapi na sisi tunaangalia kwa kuangalia ikama za shule husika au ikama za hospitali husika au zahanati au vituo vya afya husika ndiyo tunawapeleka. Ukiwaachia kule kinachotokea ni kitu cha ajabu kabisa cha tofauti sana na wengine hata hawafiki kule, ndio maana tulifanya hatua hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, endelea kutuamini tu kwa sababu bado tumefanya vizuri sana mpaka hao walimu wa sayansi ambao tumewapata, tulipowapangia, hawana option, wamekwenda mpaka kuripoti kwenye shule hizo. Ahsante sana.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna watu ambao wanasaidia kazi za uongozi kwenye nchi hii nafikiri hata kuliko sisi Waheshimiwa Wabunge na wamekuwa msaada mkubwa sana kwetu kwenye kutekeleza majukumu yetu kwenye majimbo na kwenye Halmashauri zetu ni viongozi wa Serikali za Mitaa kwa maana ya Wenyeviti wa Vijiji, lakini ambao wanafanya kazi kubwa zaidi ni Madiwani kwenye Halmashauri zetu. Hata hivyo ukweli ni kwamba unapoangalia maslahi ambayo hawa watu wamekuwa wakiyapata ni madogo sana na mara nyingine Serikali inaamua ku-temper nayo kwa makusudi kabisa hata kuingilia ule utendaji wa ndani wa Halmashauri wa moja kwa moja inapokuja suala la matumizi ya fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kila wakati tumekuwa tukihoji kwenye Bunge hili kwamba ni lini Serikali inakwenda kuboresha maslahi ya Wenyeviti wa Vijiji pamoja na Madiwani ili nao waweze kuishi kama viongozi na waonekane kwamba kweli kazi wanayoifanya inathaminika kwenye Taifa? Kila siku Serikali inasema…
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, Serikali naomba iji-commit kabisa kwamba ni lini watakwenda kuboresha kabisa haya maslahi ya wenyeviti wa vijiji pamoja na Madiwani na waache kusema tutaliangalia, tutaliangalia………..
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali tunatambua viongozi hawa wa ngazi za chini, Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vijiji na Madiwani wanafanya kazi kubwa sana katika nchi hii, maendeleo yote yanasimamiwa na wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni kweli pia kwamba maslahi ya watumishi mbalimbali wa umma pia watumishi wa kisiasa kila mmoja anasema hayatoshi, tuongeze. Hata Wabunge wanasema hivyo, walimu wanasema hivyo na wote wanasema tuongeze. Hili litawezekana endapo uchumi wa nchi utatengemaa. Katika mazingira ya sasa, kinachowezekana na ambacho sisi tunaona kinapaswa kufanywa na Serikali kwa ngazi hizi za chini ni ile asilimia 20 tunayoipeleka kwa ajili ya kuendesha ofisi, lakini pia huwa kuna posho ambayo inapatikana. Asilimia 20 ya kiasi cha shilingi bilioni moja au Halmashauri zingine zinakusanya makusanyo ya ndani mpaka shilingi bilioni 50 si hela kidogo zikigawanywa vizuri Kwa hiyo mimi niseme tu kwamba tunatambua mchango wa viongozi hawa wakati ambapo uchumi utatengemaa tunaweza tukaongeza lakini kwa sasa utaratibu ndiyo huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgawanyo wake kama tulivyosema, 40% zitakwenda kwenye miradi wa maendeleo kwenye fedha ile ya own source, lakini 10% kwa mikopo kwa ajili ya wanawake na vijana na 20% itakwenda kwa ngazi za chini na hiyo 30% itatumika katika kuendesha Halmashauri. Hii ndiyo hesabu mpya ambayo tumeiweka baada ya bajeti yetu tuliyoisoma hivi karibuni.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Vituo vya Afya vya Mwese, Karema na Mishamo ni vituo ambavyo vinahudumia wananchi wengi kwenye Jimbo la Mpanda Vijijini. Vituo hivi havina huduma ya kimsingi ya wataalam na hasa suala zima la ambulance. Naomba kujua, Mheshimiwa Naibu Waziri atavisaidia vipi hivi vituo vya afya ambavyo vinahitaji huduma ya Serikali ili kuokoa maisha ya wananchi kwenye Jimbo hilo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Kakoso kama ifuatavyo:-
Ni kweli kwamba yako mahitaji ambayo hayatoshelezi katika vituo vyetu vya afya na hospitali zetu, lakini hospitali hizi zipo kwenye Halmashauri na Halmashauri ndizo hupanga bajeti zake za kila mwaka.
Sasa nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, sehemu ya kuanzia katika kukamilisha huduma mbalimbali katika Sekta ya Afya, iwe ya elimu, mipango yote inaanzia kwenye Halmashauri. Kama watakuwa waliweka kwenye bajeti zao, basi wanaweza wakapata hizo ambulance na vifaa ambavyo pengine vina upungufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi kwa sasa hatuna mpango mahsusi wa kununua magari ya ambulance kwa nchi nzima kwa sababu, upungufu ni mkubwa, isipokuwa tunaangalia kutokana na bajeti zao za Halmashauri na sisi Serikali kwa fedha iliyopitishwa tutakuwa tumewatengea na kuwapatia fedha hizo kwa kadiri walivyoomba katika bajeti zao.
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa matatizo ya Magu yanafanana sana na matatizo ya Nyamagana, Barabara ya Ngudu – Magu – Ngumarwa, usanifu umeshakwisha kukamilika, sambamba na Barabara ya Airport – Igombe – Kayenze – Kongolo – Nyanguge ili kupunguza msongamano wa kuingia Jiji la Mwanza na kwa sababu ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, je, barabara hizi zitaanza kujengwa lini kwa kiwango cha lami? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana yanayotolewa na Naibu wangu, Mheshimiwa Jafo, napenda kujibu maswali ya nyongeza yaliyoulizwa yanayofanana sana na Waheshimiwa Wabunge juu ya ahadi za Mheshimiwa Rais ya barabara zilizoko chini ya Ofisi ya Rais TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumezihakiki, tunazifahamu lakini pamoja na mipango ya halmashauri, Wizara yangu itakuja na mpango mkakati wa namna ya kuzitekeleza barabara hizo zote kabla ya mwaka 2020. Serikali hii ni Serikali ya vitendo, tuliahidi, ni lazima tutatekeleza na ahadi za Rais ni kipaumbele chetu.
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kama alivyokwishasema Mheshimiwa Waziri kwamba mapato ya Halmashauri ndiyo vyanzo vikuu vinavyoendeleza maendeleo katika Halmashauri. Kwa kuwa makusanyo yanayotokana na mapato na kodi ya ardhi na majengo urejeshaji wake kutoka katika mamlaka husika umekuwa ukisuasua huku Halmashauri zikiwa zimejipangia majukumu mbalimbali na hivyo utekelezaji wake kuchelewa. Je, Serikali haioni kwamba mtindo huu unaathiri utekelezaji wa haraka wa vipaumbele ilivyojipangia Halmashauri? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa ndani ya Halmashauri zetu kwa mujibu wa sheria wametakiwa kutekeleza agizo la kuwawezesha wanawake na vijana kwa kutenga asilimia 10 ili ziwaendeleze kiuchumi. Kwa kuwa changamoto hii imekuwa ikiathiri sana agizo hili, je, Serikali sasa ipo tayari kuleta waraka Bungeni wa mapendekezo ya kwamba mapato yanatokana na kodi za ardhi na majengo baada ya makusanyo zibaki kwenye Halmashauri husika? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kodi za ardhi na majengo zinakusanywa kwa sehemu, kwa mfano, kodi ya ardhi inakusanywa na kupelekwa Wizara ya Ardhi na baadaye kupelekwa Hazina na hupaswa kurejeshwa kwenye Halmashauri zetu asilimia 30. Urejeshaji huu haujawa mzuri kwa muda sasa, lakini katika bajeti ya mwaka huu tunaokwenda nao katika makusanyo yaliyopelekwa karibu shilingi bilioni 29 angalau kiasi cha shilingi bilioni 4.6 kimerejeshwa, kwa hiyo, utaona tunafanya hivyo.
Hata hivyo, wakati wa hotuba yangu ya bajeti nilisema tunajaribu kuangalia na kupitia sheria hizi ili tuweze ku-harmonize ili fedha ambazo zinakusanywa zirejeshwe kwa utaratibu mzuri zaidi. Kwa hiyo, nachotaka kuahidi tu ni kwamba kwa kodi hizi zote mbili, ya ardhi na majengo, Waziri wa Fedha atakaposoma Sheria ya Fedha kwa mwaka 2017/2018 kutakuwa kuna mabadiliko ambayo yatazingatia maoni mengi ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati nawasilisha bajeti yangu lakini katika mazungumzo mbalimbali kupitia maswali ya Wahemishiwa Wabunge.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na asilimia kumi ambayo inatolewa kama mikopo kwa vijana na akina mama, tutajaribu kuangalia kama tunaweza tukaanzisha sheria mahsusi kwa ajili ya jambo hili kwa sababu kwa sasa lilikuwa limewekwa kisera tu lakini hakukuwa na sheria inayo- enforce. Hata hivyo na lenyewe tumeliweka katika utaratibu endapo tutapata fursa ya kuleta mabadiliko ya sheria mbalimbali basi tutaliweka na maandalizi yake sisi kama Wizara tayari tumekwishayafanya.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali ndogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imechukua mfumo wa kodi ya majengo kukusanywa na TRA, lakini kumekuwa na sintofahamu kubwa kwa wananchi wetu kwamba ni majengo yapi hasa ambayo yanatakiwa kulipiwa kodi katika Halmashauri zetu maana hata nyumba za tembe na udongo nazo zinachangiwa kodi. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli mwaka 2015 kupitia Sheria ya Fedha tulifanya marekebisho ya sheria na katika kifungu cha 25(2)(b) tulieleza kwamba chanzo hiki badala ya kuwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mijini kiende hata kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa zilizo Vijijini yaani District Councils. Hata hivyo, tafsiri ya mabadiliko haya haijatafsiriwa vizuri na mamlaka zenyewe kwa sababu mazingara haya yalikuwa ni mahsusi kwa maeneo kama yafuatayo; kwa mfano, Ngurdoto pamoja na establishment yote kubwa ya hoteli, facilities na kumbi za mikutano unaikuta iko vijijini, huwezi ukaacha kukusanya pale property rate au Bagamoyo yako maeneo mengi sana ya hoteli ambazo zipo vijijini, yalikuwa ni maeneo maalum kama hayo.
Mheshimiwa Spika, ili uweze kukusanya chanzo hicho ni lazima itugwe Sheria Ndogo kutoka kwenye Halmashauri husika na sheria hiyo inatungwa Waheshimiwa Wabunge mkiwa wajumbe. Unakuta inatungwa Sheria ya Ndogo ambayo kabisa inakiuka tafsiri nzuri ya sheria iliyotungwa na Bunge.
Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kueleza tu kwamba tafsiri ya kwamba ukusanyaji wa property rate sasa unakwenda mpaka kwenye vijiji kwenye nyumba za tope na udongo si sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, usahihi ni kwamba kwa mazingira maalum ya uwekezaji ambayo uko vijijini lakini unauona ni uwekezaji wa kimjini huko ndiko zinatakiwa kukusanywa. Si kwa nyumba ya mwananchi wa kawaida ambayo haiingizi kipato chochote, hajapangisha mtu yeyote, yeye anaishi tu, hatujafikia hatua hiyo kama nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuziagiza Mamlaka zote za Serikali za Mitaa ambazo zinafanya hivyo kukusanya kutoka kwenye nyumba za tope, nyumba za bati au nyumba zozote lakini ambazo haziingizi mapato, si za kibiashara na ziko vijijini, hapana, haitakiwi kukusanya na Serikali ya CCM haijaamua uamuzi huo bado. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwanza nilitaka niongezee tu kwamba kwa mwaka huu ambao tunamalizia, TRA ilikusanya kodi ya majengo kwa Halmashauri 30 tu, Halmashauri nyingine zilitakiwa kuendelea na utaratibu wa kawaida wa kukusanya mapato hayo yanayotokana na kodi ya majengo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nisisitize nchi yetu hii ili tuende ni lazima tuendelee kujenga utaratibu wa wananchi wetu kulipa kodi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. Nitatoa ufafanuzi mchana kuhusu kodi hii ya majengo na nimwombe sana Mheshimiwa Cecilia Paresso avumilie tu kidogo mpaka ile hotuba itakayowasilisha Bajeti Kuu ya Serikali mchana tutafafanua zaidi kuhusu kodi hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza nitoe shukrani kwa kupeleka madaktari wanane kwa awamu, watano halafu watatu. Hata hivyo, kuna tetesi kwamba kuna daktari mmoja atahamishwa hivi karibuni. Napenda kujua kama ni kweli na kama siyo kweli basi nipate ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kwamba kama wakimhamisha yule watatuletea tena lini daktari mwingine? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa changamoto katika Hospitali ya Wilaya ya Bukombe ni sawa kabisa na changomoto iliyoko katika Halmshauri ya Wilaya ya Geita, tuna upungufu mkubwa sana wa madaktari pamoja na wauguzi. Je, Serikali inasemaje kuhakikisha kwamba Serikali inaleta watumishi wa afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, suala la kwamba kuna tetesi za kuhamishwa hivi karibuni kwa daktari mwingine labda kwa sababu anajua ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi hawajui na labda pengine kwa sababu ya kuweka sawa niweke vizuri kwamba hata ule uhamisho wa mwanzo tulioufanya ulikuwa ni kwa sababu kulikuwa kuna shida ya kutafuta madaraka hali iliyopelekea daktari mmoja aliyekuwa anakaimu nafasi ile akashambuliwa mtaani ambapo ilionekana kama ni kutokana na mazingira hayo. Ndiyo maana tukafanya ule uhamisho na baadaye tukapeleka madaktari wengine. Kwa hiyo, kama ni tetesi zenye dhana ile ile na pengine hatua hizi zitakuwa zina sababu ile ile atahama, lakini haina maana kwamba hatutapeleka daktari mwingine kuziba nafasi hiyo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameuliza kuhusu upungufu wa madaktari kwa maeneo yote sasa siyo tu Bukombe na Geita, lakini pia najua tuna upungufu wa madaktari na wauguzi katika maeneo mengi. Mheshimiwa Rais ametoa kibali cha ajira za watumishi wengine 15,000 ambao wataziba nafasi ya hawa watumishi hewa waliokuwa na vyeti fake ambao wameondolewa. Kibali hicho kinaendelea na katika kibali hicho pia tuna idadi kubwa tu ya wataalam wa afya ambao watakuja kwa ajili ya ku-replace lakini tuna ajira zingine 54,000 ambazo ni za mwaka huu wa fedha ambazo na zenyewe tunaamini katika kufanya hivyo tutaziba eneo kubwa sana la upungufu siyo tu wa idara hii ya afya lakini pia na idara nyingine kwa ujumla wake.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sasa kutokana na vyeti feki vimeondoa kabisa watumishi wa afya katika zahanati zetu. Je, ni lini hasa hawa watumishi wataenda kuajiriwa yaani wanayo time frame kwa sababu sasa hivi zahanati zina shida katika huduma hii ya afya? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kutokana na vyeti fake, watumishi takribani 12,000 wameondolewa katika utumishi wa umma.
Hata hivyo, kibali kilichotolewa na Mheshimiwa Rais ni cha watumishi 15,000 na tunaamini kabisa kwamba hawa watakwenda kuziba. Mchakato wake ilibidi kwanza tufanye uhakiki mzuri kwamba waliotoka ni wa idara zipi na zipi, walimu ni wangapi, manesi wangapi na madaktari wangapi. Kazi hiyo tumeimaliza na tumeshakabidhi Wizara ya Utumishi na mchakato unaendelea. Bila shaka wakati wowote tunaweza tukawaingiza katika ajira watumishi hawa wapya.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Lengo la Nne la Maendeleo Endelevu ya Dunia linasema elimu bora sawa shirikishi kwa wote ifikapo mwaka 2020/2030.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu wanafunzi wamefaulu wengi sana ambao wanatakiwa waende kidato cha tano na hasa Shule za Sayansi; lakini kuna tatizo kubwa la wanafunzi wanakwenda kwenye shule hizo hakuna maabara kabisa. Serikali Awamu ya Nne ilianza hili suala la maabara.
Je, nini jukumu la Serikali kwa haraka iwezekanavyo kuhakikisha shule zote za Sayansi zinakuwa na maabara za kisasa ili tujenge Tanzania yenye uwezo wa sayansi na teknolojia?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wanafunzi wamefaulu wengi sana mwaka huu, ni kama takribani asilimia 27 ya waliofanya mtihani. Na malengo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ilikuwa kwamba tuwe tunapeleka wanaofaulu hawa wafike asilimia 20, isipungue asilimia 20. Kwa hiyo, utaona kazi nzuri imefanywa na Serikali, lakini nichukue nafasi hii kuwapongeza sana walimu wa nchi hii kwa kazi waliofanya na kusababisha ufaulu huu mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushughulikia kiasi cha wanafunzi 93,018 ambao wamefaulu kwenda kidato cha tano, tumejipanga vizuri tumepeleka kiasi cha shilingi 22,000,000,000 ili kuhakikisha kwamba tunajenga maabara. Fedha hizi zimekwenda toka kama miezi mitatu iliyopita. Ujenzi unaendelea katika shule zote za A-level na hasa zitakazochukua wanafunzi wa combination za sayansi. Ujenzi huo tunahakika kabla shule hizi hazijaanza kupokea wanafunzi utakuwa umekamilika. Kwa sasa hivi tumetawanya watu kutoka ofisini pale Idara ya Elimu, karibu kila Mkoa tumepeleka maafisa wawili kwenda kuhakikisha kwamba wanasimamia kwa haraka ili shule hizi ziweze kukamilika. Kila shule ambayo tutakuwa tunapeleka wanafunzi zitakuwa na maabara zote zinazostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumeshachukua hatua, tumepeleka fedha hizo na nipende kumshukuru Mheshimiwa Mbunge, kama kuna shule ambayo ipo katika eneo lako basi mtusaidie Waheshimiwa Wabunge wote, kwa sababu fedha zimepelekwa na ziwe kwenye Halmashauri zetu, tusimamie tuwe karibu tuhakikishe kwamba shule zile zinakamilika kabla ya tarehe moja mwezi wa saba. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Sambamba na majibu mazuri kabisa yaliyotolewa na Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, ningependa pia kumpa taarifa Mheshimiwa James Mbatia kwamba Serikali pia imeshanunua vifaa vya maabara kwa ajili ya shule hizo, kwa hiyo ujenzi utakapokamilika vifaa vipo na wanafunzi watapata vifaa. Nakushukuru.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna la ziada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa Wakuu wa Wilaya wanatumia madaraka vibaya ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini ambapo amemsimamisha kazi Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) wa Mtaa wa Mlimwa Kusini, kwa hila na ujanja na mpango wa kutengeneza. Jambo ambalo inapelekea kunakuwa na malalamiko makubwa miongoni mwa wananchi wa Mtaa wa Mlimwa Kusini ambapo ni Kiongozi wao wamemchagua na wanampenda. Je, tabia hii mbaya ya Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, ni lini ataacha kusimamisha watu kiholela? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, scenario anayoizungumzia is a very specific scenario na pengine tungeweza kuisikiliza chanzo chake, imekuwaje, ilitokeaje. Si rahisi kwa muda huu kuweza kufanya hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wote humu Wabunge tunafahamu, namna ambavyo Wenyeviti wetu wa Vijiji na Mitaa wanavyouza maeneo, wanavyoharibu mali za umma, wanavyochezea mali za umma. Kwa hiyo, kuna mambo mengi yanayotokea huko; na sisi kama nchi tumewapa madaraka hawa watu wawakilishe mamlaka ili kuhakikisha kwamba maslahi ya umma inalindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kutekeleza majukumu haya, mazingira hayawezi yakafanana, yanatofautiana kutoka sehemu moja na sehemu nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara tunayosimamia, Utawala katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, tupo tayari kupokea jambo lolote mahsusi na kulishughulikia namna ilivyo. Lakini si kweli kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya hawa wanafanya mambo ya ovyo. Wanafanya mambo ambayo yanasababisha tunakuwa na amani katika nchi hii na tunawapongeza wanafanya mambo haya katika mazingira ambayo ni tata, kwa sababu pia kuna siasa ndani, kuna mambo mengi; tuwasaidie lakini pia tulete mambo ambayo yamekwenda sio sawa ili tuweze kuyashughulikia kulingana na yalivyo. (Makofi)
MHE. WILLY Q. QAMBALO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Tatizo la mabwawa kupasuka lililopo Tabora Kaskazini linafanana kabisa na matatizo tuliyonayo kule Karatu. Bwawa la Bashay lililopo nje kidogo ya Mji wa Karatu lilikuwa chanzo muhimu sana cha maji kwa wakazi wa Kata ya Qurus hadi pale lilipopasuka wakati wa zile mvua za el- nino. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati bwawa hilo ili wananchi wa Gongali, Bashay na Qurus waweze kupata huduma hiyo muhimu ya maji?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS – TAMISEMI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Mipango yote ya Serikali lazima ianze katika Halmashauri zetu, tufanye needs assessment, tubainishe na tuweke katika mipango ya Serikali. Hata hivyo, imeonekana kwamba katika maeneo mengi mabwawa haya mengi sana yanapasuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwasihi hasa Waheshimiwa Wabunge tunaposimama katika maeneo yetu, japo kuwa si wataalam sana katika maeneo hayo lakini tuna haki ile miradi wakati inajengwa tuisimamie kwa karibu kwa sababu wakati mwingine wakandarasi wanapojenga ile embarkment haishindiliwi vizuri na hatimaye lile tuta linapasuka au spillway ya kupitisha utoro wa maji haiwi vizuri na mwisho wa siku maji yanafurika na bwawa linapasuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa ndugu yangu Mbunge wa Karatu jambo hili tumesema kwamba kama Serikali tumelisikia, lakini naomba nielekeze kama nilivyotoa maelekezo katika maeneo mengine, kule Halmashauri ya Karatu tuweke kipaumbele cha kufanya ukarabati wa bwawa hili ambalo linasaidia wananchi ili hatimaye tutenge fedha katika bajeti ile ili tuweze kurekebisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naomba niseme kwamba tumelisikia, tumelipokea na kama Serikali tunajua kuna wananchi wetu huko wanapata shida kwa sababu bwawa limepasuka.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Suala hili la hadhi ya mahabusu wetu ni suala nyeti na pana; na kwa kuwa sisi wote humu ndani tunayo nafasi ya kufanya marekebisho katika sheria hizi ili haki ya aina yoyote ya mahabusu iweze ikatendeka; na tumemsikia Jaji Mkuu akisema kwamba pamoja na kuwepo kwa wingi wa mahabusu ni kutokana na kutokufanyika kwa upelelezi na kuukamilisha ndiyo mtu aweze kupelekwa Mahakamani:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiuliza Serikali, au Serikali kama imesikia kilio cha Jaji Mkuu na ushauri wao, nasi ni Wabunge na tukitegemea tunayo nafasi ya kuweza kufanya mabadiliko ya sheria hizi sasa, maana huwezi kujua kesho, wote hapa ni wafungwa watarajiwa; iwe kwamba, kama ni miezi mitatu upelelezi haujakamilika, basi mfungwa au mahabusu aachiwe au vinginevyo kwa busara itakavyoelekeza sheria hii sasa ifanyiwe marekebisho mahabusu waweze kupata haja na haki zao za kimsingi.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa wingi wa rehema kubwa na ndogo anazotujalia sote hata kufika siku hii ya leo. Vile vile nimshukuru tena Mheshimiwa Rais kwa kuniteua kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbatia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hadi sasa jitihada hizi zinazofanyika kwa njia hizi tatu ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri amezijibu kwenye jibu la msingi ni maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, alipotembelea Magereza likiwepo Gereza la Butimba na akatoa maelekezo kwamba hali ilivyo, Magereza yamezidiwa na mahabusu ndio wengi zaidi na ndiyo maana hatua zinaendelea kuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, DPP amekuwa akifanya jitihada za kutembelea Magereza na kuongea na wafungwa. Pia nasi kama Wizara tumekuwa tukifanya hivyo na ninaamini kabisa kila baada ya muda tutakuwa tunapunguza baadhi ya mahabusu ambao wana kesi ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua kubwa zinafanyika, nami nadhani iko haja ya jitihada hizi zinazofanyika tukawa tunaleta taarifa hapa kwenye Kamati au kwa njia yoyote ambayo mtaona inafaa kwa sababu ni kweli jitihada zinafanyika. Isipokuwa mchakato wake kama mnavyofahamu, zipo haki za wafungwa, zipo haki za mahabusu na zipo pia haki za waliotendewa makosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, usilichukulie jambo hili kama ni jepesi. Lazima lichujwe, liangaliwe na upo utaratibu wa kisheria wa kufanya mambo haya. Kwa hiyo, pia tusikimbilie kushabikia tu haki za hawa waliotenda makosa. Ni kweli wanazo, lakini zipo haki pia za waliotendewa makosa. Kwa hiyo jambo hili linahitaji tuli-balance vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kwa jibu hilo watakubaliana nami kwamba jitihada hizi kwa kweli ni kubwa na zimetokana na maagizo na maelekezo ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Nashukuru kwa majibu hayo yaliyotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wananchi wengi waliofanya mambo ya muhimu na ya kuandika historia. Mfano Meja Jenerali Mrisho Sarakikya aliyepandisha bendera ya siku ya Tanganyika ilivyopata uhuru. Hivi Serikali haioni umuhimu wa kuandaa sera ya kushughulikia viongozi kama hawa ikasaidia kuamsha ari ya uzalendo kwa nchi yetu ya Tanzania kuliko kusema kwamba tutawaonea huruma, tutawatazama wako hawa na hawa? Serikali inasemaje kuhusiana na suala hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri, naomba nijibu swali la nyongeza lililoulizwa nikijumuisha pamoja na majibu yaliyotolewa kwa swali lililopita kwamba nchi hii inayo watu wengi sana waliofanya mambo makubwa katika historia ya nchi yetu na Serikali imekuwa ikitambua michango yao kwa namna mbalimbali. Hawa wanne tunaowazungumzia waliochanganya udongo wa Tanzania Zanzibar na Tanganyika na kufanya alama ya Muungano ni moja tu ya wazee wengi ambao wengine hata kuwatambua bado hatujawatambua. Wako wazee waliopigana vita ya Kagera, wako watu waliofanya shughuli mbalimbvali zilizofanya Tanzania hii ya leo tunayoiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili ni lazima tujipe tahadhari kuhusu ukubwa wake lakini pia hatuwezi tukaliacha hivi hivi ni lazima tutafakari kwamba je, tunapotaka kuchukua tuchukue kada ya namna gani au watu wa namna gani. Naomba tu niseme kwa niaba ya Serikali kwamba kwanza tunatambua na kuheshimu na kuenzi michango ya wazee waliofanya mambo makubwa hapa nchini lakini tunahitaji muda wa kutafakari sana mwisho wake yaani limitation na scope yake iwe wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kanuni ya Muasisi wa Taifa hili, Mwalimu Nyerere ni kwamba binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja. Kanuni ya utu ndiyo inayoibeba dunia leo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazee wetu wengi wamechangia Taifa hili kutokana na nyanja mbalimbali, wengine walimu, wafanyakazi wa sekta mbalimbali, madaktari, wauguzi, wakulima, kila mmoja wetu amechangia Taifa hili tukafika hapa tulipo. Nini sera madhubuti ya Serikali na iliyo endelevu kwa ajili ya kuhakikisha wazee wetu wote hawa wanapata huduma za msingi na zinazostahili kukuza utu wao na hasa huduma ya afya ambapo wazee wengi vijijini kwa kweli wanateseka sana, sana, sana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza lililoulizwa na Mheshimiwa Mbatia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tukitaka kutafuta mchango wa watu mbalimbali hapa nchini ni karibu kila mmoja ana mchango wake, awe alikuwa mwalimu ametoa mchango wake kwa sababu sisi wote tuliopo hapa tumefundishwa na walimu na si ajabu ni wazee ambao wengine wana hali mbaya. Wako madaktari, manesi na kwa neno la jumla tunalolifahamu ni wakulima na wafanyakazi wote wamechangia maendeleo na ustawi wa nchi yetu hadi ilipofika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mifano ya wenzetu wengine namna pekee ya kuwaenzi ni mfumo mzuri wa bima ndiyo huwa unaweza kuwatunza wazee hawa vizuri. Kama hatukuwa na mifumo imara sana ya bima kutafuta njia mbadala kwa sasa na kwa ukubwa wa michango mikubwa iliyotolewa haitasaidia kwa sababu huwezi kusema mkulima hakuchangia Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu ambao wamefilisika baada ya vita ya Uganda kwa sababu walitoa magari na hayakurudi. Tunahitaji kuwa na mtazamo mpana na kutafakari sana tunapokwenda huko. Ndiyo maana wakati mwingine unapofanya jambo kubwa la kujitolea kwa ajili ya nchi yako, sifa na heshima unayoipata ni kwamba wewe ni mzalendo. Neno uzalendo ni kubwa sana na pengine tumekuwa tukitambua michango ya watu mbalimbali kwa kuwapa recognition ya cheti cha Rais. Haya yote yanaonyesha heshima lakini mfumo bora na wenye kueleweka ni mfumo wa bima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwenye matibabu bora Waheshimiwa Wabunge tukatumia nafasi tuliyonayo kutunga Sheria ya Bima inayomhusu kila mwananchi awe na bima kwa ajili ya matibabu. Hii itakuwa ndiyo suluhu ya matatizo ya matibabu, ile Compulsory Health Insurance ndiyo jambo la mana nafikiri tuelekee huko tunaweza tukatatua tatizo la kuwatunza wazee wetu kwa matibabu na hata kwa mambo mengine na hasa afya zao ndiyo muhimu zaidi. Ahsante sana.
MHE. MAULID S. MTULIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nianze kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali yetu kwa kutekeleza miradi mingi iliyokuja kutatua matatizo ya wananchi, hasa katika Jimbo letu la Kinondoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya Serikali nayakubali na ni ya muda mrefu. Wakati wa bajeti Mheshimiwa Matar aliiuliza Wizara ya Fedha kwa nini miradi kama hii ambayo wafadhili wako tayari kutoa pesa inacheleweshwa? Wizara ikasema, gharama hailingani na uhalisia. Je, majibu ya Serikali ambayo ime-quote gharama ile ile ya dola milioni 120 sasa wanaona gharama hizi zinaendana na wakati na zitaenda kutekelezeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali kama inakubaliana nasi, mradi huu ni muhimu kutekelezwa. Kama inaendelea kusema gharama hizi ni kubwa, wanafanya mazungumzo kuja kwenye gharama halisi au wanachagua kuweka wawekezaji wa ndani ili bonde hili lipate kujengwa na wananchi walipe fidia wapate kuishi maisha bora?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, gharama hizi ndizo gharama ambazo zimeandikwa kwenye andiko. Andiko lile ni zito na kubwa sana na bado mchakato unaendelea kwa sababu, keshokutwa mimi mwenyewe nitapokea uwasilishaji wa andiko hilo kutoka kwa wadau hawa waliolitayarisha.

Mheshimiwa Mwenyeikiti, ni kitu kizuri kwa kweli na ni kitu kikubwa sana. Kwa hiyo, ndani ya Serikali lazima tupewe muda wa kuchakata ili tuweze kutoka na kitu kizuri kwa sababu kusema ukweli gharama hizi pamoja na kwamba zinaonekana kubwa, lakini pia ni lazima tuone kwamba na huu Mto Msimbazi ni mrefu, lakini pia unaweza kugeuzwa badala ya kuwa tatizo ukawa na fursa kubwa kama nilivyosema kwamba kutakuwa kuna parking, kutakuwa kuna ma-conference na vitu vikubwa vingi sana ambavyo vitajengwa kando kando ya Mto Msimbazi, lakini pia kutunza ikolojia na kuleta ladha na uzuri wa maeneo ya Mto Msimbazi kuanzia mwanzo wake mpaka mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu gharama kwamba ni zile zile, ni kweli, bado mpaka sasa ni zile zile, lakini mchakato ndani ya Serikali unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake kwamba kwa kuwa, gharama ni zile zile sasa je, Serikali iko tayari? Ni kwamba Serikali kwa maana ya uzuri wa mradi iko tayari, lakini suala la fedha ni suala ambalo pia linahusika na Wizara ya Fedha. Nasi bado tunaendelea na mchakato katika eneo letu na baadaye taarifa hii tutaikabidhi na ikibidi hata kuja kufanya uwasilisho hapa Bungeni ili Wabunge muweze kuona na pengine wananchi nao waweze kujua namna ambavyo kwa kweli Mto Msimbazi na Dar es Salaam itakavyokuwa baada ya utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba wananchi wa Dar es Salaam, kama walivyoshiriki vizuri katika uandaaji wa mradi huu, basi tuendelee kushirikiana na wawe wavumilivu kwa sababu hili jambo siyo dogo, ni kitu kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Matatizo haya ya Mto Msimbazi yanafanana sana na matatizo yaliyopo maeneo ya Hananasifu. Sasa je, Mheshimiwa Waziri kwa kuwa World Bank wako tayari kutupatia fedha kwa ajili ya kuondoa matatizo haya ya mafuriko katika mto ule: Je, ni lini sasa Serikali itaridhia hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, utayari wa Benki ya Dunia ni jambo moja, lakini uhalisia wa gharama pia ni jambo jingine, kwa hiyo kama Serikali siyo kwamba ni Serikali inayopokea pokea offers tu ni lazima tuangalie kwamba tunachokipokea kina tija na je gharama yake ni sahihi? Kwa hiyo, nipende tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kama Serikali tuna nia ya kutekeleza mradi na andiko liko tayari na kwa kweli wadau wanaojitokeza siyo World Bank tu wako na wengine wanaojitokeza wengi lakini lazima tutafakari na kuangalia uhalisia wa gharama, Hivyo nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali itafanya uwekezaji lakini kwa kuangalia uwezo wa uchumi wa nchi yetu lakini pia na aina ya msaada tunaoupokea.
MHE. YUSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika mvua za masika za mwaka jana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alisema kwamba tayari Serikali imepata mfadhili na watajenga mto Msimbazi badala ya kuwa adhabu itakuwa ni starehe kubwa kwa sababu utakuwa ni kivutio kikubwa cha utalii kwa mkoa wa Dar es Salaam. Leo Mheshimiwa Waziri anasema bado kuna mchakato. Je, Serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam ilikuwa ina mradi wake na Serikali Kuu ina mradi wake au ni huo huo mmoja hamjakubaliana?(Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu yote kuanzia jibu la msingi na haya ya nyongeza, nimesema Serikali iko tayari na ina mpango wa kutekeleza mradi huu na ndiyo maana tumesema mradi huu utakuwa kivutio kikubwa utakayoipamba Dar es Salaam na kuwa Dar es Salaam nzuri sana kwa sababu ni mradi ambao ukisharekebisha Bonde la Mto Msimbazi kwa ukubwa wake, na kuweka parking za magari conference centers lakini pia maua na vitu kama hivyo basi maana yake ni mradi ambao utakuwa umeipamba Dar es Salaam na hivyo kauli ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kwamba Dar es Salaam itakuwa nzuri na Msimbazi itakuwa nzuri, bado inabaki pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachozungumzia hapa ni kumalizia mchakato wa kutafuta fedha, offers zipo lakini kama Serikali lazima tufanye utaratibu kwa kuzingatia sheria ya misaada na mikopo ili tuweze kupata mikopo au msaada ambao una tija, hapa ndipo tunaposema gharama hizi zilizoandikwa bado ni mapendekezo, lakini kama Serikali tunamalizia mchakato wa kuhakikisha kwamba tunatekeleza mradi huu. Kwa hiyo, mradi upo na utatekelezwa lakini Serikali lazima ijiridhishe na offers tunazozipewa. (Makofi)
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza, nione tu kwamba bahati mbaya sana Mheshimiwa Waziri hakujibu swali langu na badala yake ameenda kuzungumza vitu vingine. Nilichokiomba mimi ni kuona kwamba busara ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano inatumika na kuona suala la Bahari Kuu sasa Zanzibar wanalitekeleza kama Zanzibar kwa sababu ya kuendeleza uchumi wa Zanzibar hicho ndiyo ambacho kwamba nimekiuliza mimi. Bahati mbaya ameenda kujibu masuala ya sheria na vitu vingine. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar ni Visiwa na Bahari Kuu ni Sehemu ya rasilimali yake kubwa ambapo kama itawekezwa vizuri ina uwezo wa kuchangia kwa kiasi kikubwa kwa zaidi ya asilimia 50 kwenye uchumi wa Zanzibar na kwa sababu ni Visiwa ambavyo vimezungukwa na bahari. Je, ni mkakati gani wa Serikali kuisaidia sasa Zanzibar ili eneo hili la Bahari Kuu litumike vizuri na kukuza uchumi mahsusi hasa kwa upande wa Zanzibar?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba tu Mheshimiwa Waziri anijibu hii taasisi ambayo ipo kwanza ni taasisi gani na imesaidia kwa kiasi gani kuchochea uchumi hasi kwa upande wa Zanzibar toka kuanzishwa kwake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ningetaka kulijibu swali kama lilivyoulizwa ningeishia kusema tu Serikali haiko tayari kuondoa eneo hili la uvuvi wa Bahari Kuu kwa upande wa Zanzibar ikaachiwa kwa sababu ningekuwa nimejibu. Lakini nimeelezea msingi wake kwamba msingi wa hili ni wa Kimuungano zaidi kwa sababu kwenye sheria ile ya Kimataifa inatambulika kama ni sheria ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika International Law.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi nini Zanzibar inanufaika? Kwa kweli, manufaa ni makubwa toka tulipobadilisha na kuleta hii sheria ambapo kwa sasa itaasisi katika mapato yanayopatikana katika uvuvi wa bahari ile exclusive economic zone basi asilimia 50 inayopatikana yale mapato yanaweka katika ile taasisi ya Kimuungano na makubaliano kwa sasa katika hatua ya mpito ni kwamba asilimia 50 inayobakia ndiyo itagawanywa kati ya Zanzibar asilimia 40 na Tanzania Bara asilimia 60.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi hapa hata ile sheria yenyewe ambayo ilipitishwa bado wenzetu wa Zanzibar Baraza la Wawakilishi hawajaiorodhesha. Kwa hiyo, kama wakiiorodhesha ndipo mnaweza tukaendelea tukatoka kwenye mpito tukaja kwenye mazungumzo halisi ya namna gani sasa hoja zingine kama hizi zinaweza zikaja. Kwa hiyo ni vizuri kwanza ikaorodheshwa halafu ndiyo tuendelee kuzungumza namna ya utekelezaji wa suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maelezo haya ninadhani rafiki yangu Kombo nimemjibu uzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa ili tatizo la mlundikano wa pikipiki kwenye Vituo vya Polisi liko katika mikoa mingi, lakini utaona vijana wengi ambao wanakamatwa kuna wengine ambao hawana makosa yale ya kusema kwamba pikipiki ziwekwe kituoni. Hata hivyo, kuna wengine wameenda kukopa benki ili kama ni ajira kwa vijana, sasa wasema kwamba lazima miezi sita. Sasa ni kwa nini kusiwepo na kitengo maalum kwa sababu limeonekana hili ni tatizo karibu nchi nzima, cha kushughulikia hili tatizo la ukamataji wa bodaboda ili pengine kipindi kiwe kifupi miezi miwili au mitatu kwa sababu mengine ni makosa ambayo sio makubwa sana ya kuweka mpaka miezi sita na wengine wamepata ajali wamekufa na wengine wako hospitali? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana yaliyotolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa almaarufu Chilo, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kabati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na matukio ya mengi yanayotakana na namna ya uendeshaji wa biashara yenyewe ya bodaboda lakini pia industry nzima hiyo ukilinganisha na hatua zinazochukuliwa katika kupambana katika kuweka utaratibu wa kufuata sheria katika kufanya biashara yenyewe ifanyike lakini pia usalama wa watu.

Mheshimiwa Spika, moja kati ya vyombo vinavyotumika sana kwa sasa kufanya uhalifu ni pikipiki kuliko hata magari na kwa hivyo kumekuwa na sababu tofauti tofauti ambazo zinapelekea ukamataji na wenyewe kuwa mkubwa. Wengine wengi ni rahisi akienda kufanya tukio lenye thamani kubwa au akapora au akafanya nini kuitelekeza pikipiki ni jambo jepesi, kwa hiyo tunajikuta tuna pikipiki nyingi ziko mikononi mwa polisi, lakini wahusika ama hawajulikani walipo wamezitelekeza na ndio maana zinaitwa mali zilizookotwa.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, kwa sababu concern ya Waheshimiwa Wabunge ni kubwa kwenye jambo hili na kwa sababu pengine sababu hizi tatu zilizotolewa katika jibu letu la msingi zinaonekana hazikuwatosheleza Waheshimiwa Wabunge, acha tukafanye tathmini ya kina na tutakuja na matokeo haya tueleze kwa kina katika pikipiki zilizokamatwa nchi nzima zilizopo kwenye Vituo vya Polisi ni ngapi; na ngapi zina tatizo gani na ngapi zina tatizo gani.

Mheshimiwa Spika, kwa hatua ya muuliza swali la msingi kwamba tuone utaratibu wa kuzi-dispose kwa sababu tumesimamisha uchumi na yenyewe ni hoja ambayo ni valid. Tutakachokifanya katika tathmini hiyo tutaona kama tutapata wale waliopo husika, ili tuweze kuzipiga mnada. Kwa hiyo, nadhani tupewe muda, twende tukafanye tathmini ya jambo hili na baadaye tutoe matokeo yake hadharani.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri na Waziri lakini tumeona kwamba pamoja na faini ya bodaboda kuwa kubwa, lakini bado matukio ya uhalifu yameongezeka kwa hiyo ni ishara kwamba faini haiwezi kuzuia uhalifu, lakini ukiangalia pia katika utaratibu wa kawaida sasa hivi tuna changamoto kubwa ya ajira katika nchi yetu na Serikali yetu imeahidi kutoa ajira milioni nane na miongoni mwa watu ambao wanajiajiri sehemu yao ni bodaboda.

Mheshimiwa Spika, nadhani ni vizuri sasa Wizara ya Mambo ya Ndani ikaleta utaratibu hapa ili tuweze kupitia upya mchakato wa faini hizi kwa sababu tunafahamu mtu leo ukiua una adhabu yake, lakini pia leo mtu ukiiba kuku una adhabu yake, haiwezekani gari ambalo ni milioni mia tatu faini yake elfu thelathini na pikipiki ya milioni mbili faini yake elfu thelathini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa tunasema elfu thelathini kama ni kosa ni moja, bodaboda anaweza kupigwa makosa manne kwa siku akalipa laki na ishirini na pikipiki ile sio ya kwake, inabidi pia apekeleke hela kwa mwenye pikipiki na yeye pia aweze ku-survive. Nadhani Serikali iwaangalie kwa jicho la huruma watu hawa wa bodaboda ili changamoto iweze kuondoka.

Mheshimiwa Spika, swali langu katika eneo hili tumeona watu wa traffic wamekuwa kwa kiwango kikubwa wanawakamata sana bodaboda pamoja na watu wa bajaji. Je, Wizara ya Mambo ya Ndani ina mpango gani wa kutoa maelekezo mahususi kwa watu wa traffic ili sio kila kosa analokamatwa nalo mtu lazima apigwe faini waweze kutoa onyo pamoja na utaratibu mwingine?

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa kukijitokeza baadhi ya askari wetu kutokuwa waungwana. Unajua shughuli hizi huwezi ukazi-control kwa sheria per se a hundred percent. Kwa hiyo, hekima, busara na hasa unapokuwa mtumishi wa Umma unayewatumikia watu lazima utumie hekima na busara. Enforcement a hundred percent na yenyewe huwa kidogo ina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge, lakini pia na Waheshimiwa Wabunge mtusaidie, baadhi ya vijana wetu wanafanya kusudi na ninyi wenyewe mashuhuda, mnaendeshewa vibaya sana bodaboda hata hapa mjini, tukiacha hii hali na yenyewe ni shida pia. Mimi niseme tu, sote tutekeleze wajibu wetu na kwa upande wa askari polisi, hasa wa usalama barabarani wajitahidi kuwa wanatumia busara katika kuhakikisha kwamba wanasimamia sheria siyo kukomoa.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naona kijembe kimeingia sawasawa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nami niwapongeze kwa sababu Simba Sports Club wameisadia Tanzania kuonekana vizuri. Pia ule utaratibu wa kuitangaza Tanzania, “Visit Tanzania”, kusema kweli ni jambo ambalo linafaa kuigwa hata na wenzetu wa Young Africans pindi watakapopata nafasi ya kuingia katika mashindano haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu ni jepesi sana kuhusiana na bodaboda. Ni dhahiri kabisa biashara…

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, umesikia maoni ya Mheshimiwa; muige mambo mazuri tunayofanya. Mheshimiwa endelea. (Kicheko)

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, biashara ya bodaboda ni nzuri sana kwa vijana wetu. Pale Dar es Salaam bodaboda wanafanya vitu ambavyo vinasababisha abiria ambao ni raia wa Tanzania, ni very innocent, wapate ajali, kupoteza miguu, mikono na wengine maisha yao kwa kupita kwenye alama za taa nyekundu bila kujali, kupita no entry bila kujali, kupita katika barabara za mwendokasi bila kujali na mambo haya yanafanyika mbele ya askari wa usalama wa barabarani. Je, ni lini Serikali itasimamia kidete kuhakikisha kwamba biashara hii inaendeshwa kwa utaratibu wa kisheria ili kupunguza na kuondoa ajali ambazo zinawafika watu wetu?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hawa madereva wa bodaboda kwa kweli ni shughuli kubwa kuwasimamia. Sheria hairuhusu ku-overtake kushoto lakini ukiangalia wote utadhani wana chuo walichojifunza ambapo wamefundishwa ku-overtake kushoto. Nafahamu kwa nini wanafanya hivyo; wanafanya hivyo kwa sababu ku-overtake kulia wanakuwa kati ya gari moja na nyingine, si salama zaidi kwao. Madereva wa magari mtu aki-overtake kushoto jicho lako linakuwa kulia zaidi, ni rahisi kama unakwenda kushoto ukaingia bila kutazama, ndiyo ajali nyingi zinatokea kwa sababu hiyo.

Mheshimiwa Spika, niseme tu, bado tuna kazi kubwa. Nami niwaagize tu Jeshi la Polisi Kitengo cha Traffic kuhakikisha kwamba madarasa yanafanyika ili kutoa elimu kwa sababu watu hawa tunawahitaji. Kuna graduates wanaendesha bodaboda, kuna watu wa masters wanaendesha bodaboda, kwa hiyo, siyo industry ya kuidharau, ni industry inayofanywa na watu wanapata riziki yao, lakini tuwaombe sana kwamba wazingatie sheria kwa sababu wanazifahamu lakini wanafanya kusudi. Jeshi la Polisi upande wa traffic wahakikishe wanatoa elimu kama tunavyofanya katika utoaji wa elimu ya usalama barabarani kwenye vituo vya bodaboda, wafundishwe namna ya kutumia chombo cha moto.

Mheshimiwa Spika, jambo hili nadhani liwe concern ya sisi sote kwa sababu kundi hili ni kubwa, askari wetu ni wachache, hawawezi wakafanya kwa kila mahali. Matajiri wa hizi bodaboda wako na humu ndani, kila mmoja akitekeleza wajibu wake tunaweza angalau kupunguza vifo vya hawa vijana, nguvu kazi kubwa ya Taifa inapotea. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kufuatana na majibu ya Naibu Waziri anasema kwamba mahabusu wana hiari ya kufanya shughuli mbalimbali; kwa sababu mahabusu wengi wanakaa muda mrefu Gerezani; miaka mitatu, nane, wengine mpaka tisa, wengine mpaka 12: Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kupeleka vifaa mbalimbali ambavyo watakuwa wanajiendeleza mle ndani kama ni kushona cherehani; yaani ujuzi mbalimbali wakiwa mle mle ndani, siyo kwenda kufanya kazi nje, kwa kipindi ambacho wanasubiria kesi zao kama zimemalizika wameachiwa huru au kama wamefungwa. Kwa kipindi hiki, kwa nini msipeleke waendeleze ujuzi wao wakiwa mle gerezani? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, Mheshimiwa Hamza Chilo, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mahabusu hawapaswi kufanya kazi kwa mujibu wa Kanuni za Kimataifa na pia sheria za nchi yetu. Hata hivyo, uzoefu unaonesha kwamba katika maeneo ambayo tumepita na kuangalia, wengine wanapenda kufanya zile shughuli za hiari yao kabisa na wanapenda kufanya kazi. Nakubaliana na Mheshimiwa Matiko kwamba katika maeneo ambako tumekuwa na shughuli ambazo haziwaruhusu kutoka nje, kwa sababu mahabusu wanategemeana na aina ya kosa alilolikosa.

Mheshimwia Spika, kwa makosa ya kawaida unaweza kumruhusu hata kutoka kidogo, lakini kwa makosa yale magumu, makubwa, siyo rahisi kumruhusu. Sasa katika maeneo ambayo tumefungua bakeries kwenye maeneo ya Magereza na Shule za Kushona ambazo ziko ndani ya Magereza, kwa kweli wanazifurahia na wanafanya.

Mheshimiwa Spika, tunachukua maoni yake hapa kwamba hicho anachokisema ndicho kinachofanyika hata kwa sasa. Tutajitahidi tu kuongeza uwekezaji kuhakikisha kwamba tunapeleka mashine hizo za kushona au zinazofanana na shughuli za kawaida zinazoweza kufanyika ndani ya Magereza ili waweze kujishughulisha kwa sababu kusema ukweli mtu kukaa bila kufanya shughuli yoyote kwa muda mrefu inakuwa siyo jambo ambalo kibinadamu linakubalika. Hata wao unaona kabisa nimesema nao, wanasema tuleteeni shughuli za kawaida tufanye. Kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa nafasi ya swali la nyongeza, lakini niseme sijaridhika kabisa na majibu ya Serikali. Changamoto hii ipo tangu mwaka 78 ambapo sasa hivi ni takribani miaka 43 mpaka leo. Nilivyotumwa na wananchi wa Nkenge kuja kuleta malalamiko ya wananchi mwezi wa saba ndipo timu ikatumwa.

Mheshimiwa Spika, unaweza ukaona majibu ya Serikali. Anayelalamikiwa ni Wizara ya Ulinzi, ameenda yeye na JKT, hakuna kuhusisha Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, hakuna kuhusisha halmashauri, hakuna kuhusisha Mbunge aliyeleta malalamiko, hatuoni nia ya dhati ya kuweza kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, swali langu la msingi, kama ni kweli tunatambua kazi nzuri ya jeshi letu, Wizara ya Ulinzi kama ni kweli wanahitaji hilo eneo kuna utaratibu wa kuchukua eneo. Na swali langu la msingi lilikuwa ni hilo, kama linatakiwa kuchukuliwa na jeshi letu la ulinzi na usalama kwa nini wasifuate taratibu za Serikali ili eneo hilo basi lichukuliwe kwa mujibu wa taratibu? Hilo ni swali langu la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Anaposema kwamba, hilo eneo halitagawiwa kwa wananchi:-

Mheshimiwa Spika, siamini kama hiyo timu waliyounda ilienda site kwa sababu, wananchi wanaishi katika eneo hilo miaka 43 iliyopita. Sasa maana yake leo katika swali langu la pili atuambie hao wananchi walioko katika eneo hilo watapelekwa wapi? Nakushukuru.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, maeneo kama haya ambayo yanashika historia, lakini pia tunafahamu kwamba, eneo hili linalosemwa ndio lilitumika kama base dhidi ya Vita ya Kagera mwaka 78. Lakini tunafahamu pia madhara makubwa na madhila makubwa waliyoyapata watu wa Kagera na hususan wa maeneo haya. Maneno haya ya Mheshimiwa Mbunge na concern anayoiweka hapa inanifanya nitafakari zaidi na niombe kwa ruksa yako, acha tuchukue maoni yake na twende tukatafakari zaidi namna bora zaidi ya kutekeleza jambo hili kwa maslahi ya nchi, lakini kwa maslahi pia, ya watu wetu walioko katika eneo hili. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata majibu ya Serikali, lakini sina raha na haya majibu, naomba kuuliza maswali mawili.

Kwa kuwa wakati wa Bunge la Kumi nilishauliza hili swali mara mbili, kwa sababu hili gari limekuwa bovu kwa muda mrefu; je, Serikali mnavyonijibu leo mko serious kweli hili gari litatengenezwa na litatengenezwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hivi Serikali inafahamu kwamba hiki Kituo cha Polisi kipo Mahore na Mahore ni tambarare na asilimia 68 ya wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wanaishi milimani na kama kituo kile kinakuwa hakina gari wale wananchi hawana ulinzi na maisha yao.

Je, Serikali mnalijua hilo na kama mnalijua mtafanya jitihada ya kutengeneza hili gari? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Same Mashariki kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba gari hili ni bovu na ni kweli kwamba ni muda mrefu, lakini ni ukweli pia ambao Mheshimiwa Mbunge hajausema. Gari hili alipewa baada ya yeye kutoa gari kwa Jeshi la Polisi aliyekuwa amepewa msaada na wafadhili wake, kwa ajili ya kituo hiki. Sasa kwa sababu gari lile aliyekuwa la kwake aliyekuwa amepewa lilikuwa la kisasa sana ambalo kwa kweli lisingeweza kupelekwa kule kijijini, Makao Makuu ya Jeshi la Polisi walilibakiza kwa ajili ya shughuli za Makao Makuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo hii Mbunge anaposikitika hivi mbele yako niseme tu kwa niaba ya Serikali na Wizara tutaitengeneza hili gari mapema iwezekanavyo ili kutoa heshima na shukrani kwa Mheshimiwa Mbunge, lakini kwa nia njema tu ya kufanya ndugu zetu wale wa Same Mashariki, kule Mahore wapate huduma hii vizuri zaidi. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ucheleweshaji wa kesi kwa kiasi kikubwa unatokana na upelelezi kutokamilika kwa muda muafaka, na kwa kuwa kuna kesi ambazo, kwa mfano, kuna kesi moja mahabusu amekaa zaidi ya miezi 8, house girl kaiba sijui vitenge viwili kwa mwajiri wake, kesi haikamiliki. Swali langu ninataka kujua; kwa kuwa kesi zinakuwa hazikamiliki, watu wanakaa miaka 8, 10 mpaka 12. Ni kwa nini sasa upelelezi usifanyike ukikamilika sasa, ikifikia hatua ya usikilizaji ndipo watuhumiwa waweze kupelekwa mahakamani, ambapo ndipo itachukua muda watu wasikae magerezani? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa si kila kesi mtuhumiwa anatakiwa kukaa mahabusu, ni baadhi ya kesi ambazo zimetajwa kwa mujibu wa Sheria, kwamba kwa makosa ya aina hii mtuhumiwa hapaswi kuachwa huru. Anatakiwa azuiwe kwa sababu kwanza yeye mwenyewe anaweza akahatarisha maisha yake kutokana na nature ya kosa alilokosa, lakini pili akiwa nje anaweza akaharibu upelelezi, kwa maana ya kesi husika kulingana na hukumu na ukubwa wa kesi yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa ambao wanatuhumiwa kubaki kwa kesi ya vitenge kama anavyosema, hii ni kesi tofauti na pengine ni kesi moja kwa nyingine. Nitoe rai na niseme tu kwamba, kwa yale makosa ambayo, na wewe unafahamu, yanahitaji kabisa dhamana na dhamana ni haki ya mshitakiwa; lakini kwa makusudi tu inazuiwa kutolewa dhamana na sheria inasema kosa hilo linadhaminika; kwamba hiki kitendo hakikubaliki na ni lazima tufuate sheria, sote tuondoe mahabusu kuwa wengi kwa kufanya hivyo. Kwa sababu, kwa kufanya hivyo kutatusaidia sana kupunguza idadi ya mahabusu wengi tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme tu, Serikali hata mara moja, lakini pia hata Idara ya Upelelezi ndani ya Jeshi la Polisi haiwezi hata mara moja ikarefusha upelelezi kwa kesi ambayo inahitaji kumalizwa upelelezi wake. Bali kama kuna jambo limetokea mimi niletewe tushughulikie. Kama kuna kesi ya khanga, kesi ya vitenge, kesi ya bakuli amefanya house girl akakaa miezi minane, ni jambo maalum la kushughulikiwa na nitaomba Mheshimiwa Mbunge tuonane naye ili aweze kunipa taarifa zaidi. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa heshima naomna niseme maneno machache kabla sijauliza maswali yangu ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, inasikitisha Serikali inapoacha migogoro inakua miaka na miaka na hili suala sio mara yangu ya kwanza kuuliza humu Bungeni, Mheshimiwa Masauni alipokuwa Naibu Waziri alijibu majibu ya hivyo hivyo. Kwa hiyo, naomba Wizara ikasome mafaili yake ya maswali itakuta ni hayo hayo majibu ni hayo na maswali ni hayo. Maswali yangu ya nyongeza ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mgogoro huu umedumu tangu mwaka 1998 baada ya mipaka iliyokuwa halali kuondolewa na kupunguza maeneo ya wananchi ya kulima na kufuga mifugo yao, nini kauli ya Serikali kuhusu kumaliza mgogoro huu? Naomba Serikali itoe kauli yake lini inamaliza mgogoro uliodumu tangu mwaka 1998?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kama kweli Serikali ina nia ya kumaliza mgogoro huu ambao unawasikitisha sana wananchi wa Ukondamoyo na Tumaini, je, Waziri yupo tayari twende naye akaone yeye mwenyewe na ndiyo atakuja kuthibitisha kama kweli majibu yanayotolewa na Serikali ni ya halali? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu na naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge yote mawili kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kama ulivyosema kwamba majibu ya msingi ya Serikali, mgogoro unaonekana haupo, ushahidi wa namna ambavyo Magereza walitoa lile eneo na kuligawanya kwa idadi ya heka ambapo Kijiji cha Tumaini kilipata heka 505, maelezo haya yanaonekana Mbunge hakubaliani nayo, ninaomba nikuhakikishie kwamba nipo tayari baada ya Bunge kwenda nikajionee mwenyewe na kuwasikiliza wananchi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. STANSALUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa Magereza nyingi zipo katikati ya mji kwa mfano Mji wa Maswa ipo katikati ya mji na majengo na maeneo yao yanaingiliana sana na makazi ya watu na maeneo hayo yanaonekana kuwa ni potential hata kwa uwekezaji mwingine.

Je, ni lini Serikali itaamua basi kujenga Magereza nje ya miji kwa mfano Maswa tumeshatoa na eneo na kuwapa Magereza ili wajenge nje ya mji na kuachia maeneo ya katikati ya mji kwa ajili ya uendelezwaji wa shughuli zingine za kibiashara? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyongo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa asili zamani huko kidogo maeneo haya yalikuwa pembeni ya miji, lakini kadri miji inavyokua tumejikuta sasa wakati mwingine maeneo haya ya Magereza na hata majeshi yakiwa katikati ya miji, jambo hili sio la kulijibu kwa haraka haraka kwa sababu ni mpango mkubwa unaohusisha Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Magereza au vyombo kama hivyo ambavyo vina changamoto kama hiyo.

Mheshimiwa Spika, wacha tulichukue tuone namna tunavyoweza kulifanya lakini si jambo jepesi kwa haraka kuhamisha gereza kwa mara moja na miundombinu yake, uwekezaji uliopo pale ni mkubwa lakini ni hoja ambayo kwa kweli Mheshimiwa Mbunge acha tuichukue tuitafakari.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa heshima naomna niseme maneno machache kabla sijauliza maswali yangu ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, inasikitisha Serikali inapoacha migogoro inakua miaka na miaka na hili suala sio mara yangu ya kwanza kuuliza humu Bungeni, Mheshimiwa Masauni alipokuwa Naibu Waziri alijibu majibu ya hivyo hivyo. Kwa hiyo, naomba Wizara ikasome mafaili yake ya maswali itakuta ni hayo hayo majibu ni hayo na maswali ni hayo.

Maswali yangu ya nyongeza ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mgogoro huu umedumu tangu mwaka 1998 baada ya mipaka iliyokuwa halali kuondolewa na kupunguza maeneo ya wananchi ya kulima na kufuga mifugo yao, nini kauli ya Serikali kuhusu kumaliza mgogoro huu? Naomba Serikali itoe kauli yake lini inamaliza mgogoro uliodumu tangu mwaka 1998?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kama kweli Serikali ina nia ya kumaliza mgogoro huu ambao unawasikitisha sana wananchi wa Ukondamoyo na Tumaini, je, Waziri yupo tayari twende naye akaone yeye mwenyewe na ndiyo atakuja kuthibitisha kama kweli majibu yanayotolewa na Serikali ni ya halali? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu na naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge yote mawili kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kama ulivyosema kwamba majibu ya msingi ya Serikali, mgogoro unaonekana haupo, ushahidi wa namna ambavyo Magereza walitoa lile eneo na kuligawanya kwa idadi ya heka ambapo Kijiji cha Tumaini kilipata heka 505, maelezo haya yanaonekana Mbunge hakubaliani nayo, ninaomba nikuhakikishie kwamba nipo tayari baada ya Bunge kwenda nikajionee mwenyewe na kuwasikiliza wananchi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. STANSALUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa Magereza nyingi zipo katikati ya mji kwa mfano Mji wa Maswa ipo katikati ya mji na majengo na maeneo yao yanaingiliana sana na makazi ya watu na maeneo hayo yanaonekana kuwa ni potential hata kwa uwekezaji mwingine.

Je, ni lini Serikali itaamua basi kujenga Magereza nje ya miji kwa mfano Maswa tumeshatoa na eneo na kuwapa Magereza ili wajenge nje ya mji na kuachia maeneo ya katikati ya mji kwa ajili ya uendelezwaji wa shughuli zingine za kibiashara? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyongo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa asili zamani huko kidogo maeneo haya yalikuwa pembeni ya miji, lakini kadri miji inavyokua tumejikuta sasa wakati mwingine maeneo haya ya Magereza na hata majeshi yakiwa katikati ya miji, jambo hili sio la kulijibu kwa haraka haraka kwa sababu ni mpango mkubwa unaohusisha Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Magereza au vyombo kama hivyo ambavyo vina changamoto kama hiyo.

Mheshimiwa Spika, wacha tulichukue tuone namna tunavyoweza kulifanya lakini si jambo jepesi kwa haraka kuhamisha gereza kwa mara moja na miundombinu yake, uwekezaji uliopo pale ni mkubwa lakini ni hoja ambayo kwa kweli Mheshimiwa Mbunge acha tuichukue tuitafakari.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na nitaomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwanza ni ukweli kwamba tunajua umuhimu wa kazi ya Idara ya Uhamiaji katika kusimamia masuala aliyoyasema Mheshimiwa Waziri ya ungiaji wa wageni ukaaji wao. Hata hivyo, kiwango cha usumbufu wa wananchi unaotokana na doria za uhamiaji kimepita kiasi ambacho sisi tunakifahamu katika historia ya Mkoa wetu wa Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Mheshimiwa Waziri aniambie kuna jambo lipi jipya ambalo limejitokeza linalosababisha kwa sasa kuwe na misako inayosumbua hata raia halali waliokaa katika mkoa wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili; msingi wa kukua kwa tatizo hili ni kuchelewa kwa Wizara yake kutoa vitambulisho vya NIDA kwa wananchi halali wa Mkoa wa Kigoma, jambo ambalo lingekuwa limekamilishwa, haya yote yasingekuwepo. Anieleze ni lini Serikali itakamilisha kazi hii ya kutoa vitambulisho vya NIDA ili kuondokana na usumbufu huu; na kama inawezekana misako hiyo isimame mpaka hapo mtakapokamilisha vitambulisho vya NIDA? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kiwango cha usumbufu katika kusimamia Sheria ya Uhamiaji, Kifungu cha 12 kama ilivyorejewa mwaka 2016 ambapo Jeshi la Uhamiaji limepewa jukumu la kufanya misako, doria na hata ikibidi kufanya upekuzi ili kubaini nani ni raia na nani sio raia; zoezi hili kama tulivyojibu katika jibu letu la msingi, linafanyika kwa nchi nzima. Usumbufu huu unatokana na mkoa ulivyo na mipaka na majirani zetu ambapo mara nyingi kumekuwa kuna shida katika nchi zao na kwa hiyo wana msukumo mkubwa sana wa kuja katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kusema kweli kwa muda wa miezi mitatu tumekamata wahamiaji haramu zaidi ya 1,000. Kiwango hiki ni kikubwa na siyo rahisi tusifanye doria, lakini tunafanya hivyo kwa mikoa yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anauliza vitambulisho vya NIDA vingetotewa basi usumbufu usingekuwepo. Ni kweli, lakini nataka niseme, kupewa kitambulisho cha NIDA cha uraia wa Tanzania siyo mwarobaini kwamba wewe sasa huwezi ukaulizwa kuhusu uhalisia na uhalali wa uraia wako. Sheria hizi ni mbili tofauti; kuna Sheria ya Uraia, Sheria ya Uingiaji Nchini na Sheria ya Vitambulisho vya Taifa na zote hizi zinashughulikia mambo mawili tofauti. Vitambulisho hivi hata wakazi wasio raia wanapewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna madaraja tofauti tofauti ya kutoa vitambulisho. Siyo kwamba ukipewa kitaambulisho hiki, basi wewe hutaulizwa tena. Tutaulizwa, hata mimi naweza nikaulizwa uraia wangu hata kama nina kitambulisho na hata kama natoka Dodoma; nitaulizwa uraia wangu na uhalisia endapo utajitokeza wasiwasi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ndiyo majibu yetu ya Serikali na tunaomba Mkoa wa Kigoma watuelewe hatufanyi kwa Mkoa wa Kigoma peke yake, tunafanya kwa mikoa yote. Hivi sasa kuna oparesheni imeanza tarehe mosi itaisha tarehe 15 ya mwezi huu kwa mikoa yote ya Tanzania. (Makofi)
MHE. HAJI MAKAME MLENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza swali moja tu la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Jimbo la Chwaka lina kituo kingine kidogo cha Polisi kilichopo Jozani: Je, Serikali haioni kwamba kuna sababu ya kukipelekea usafiri angalau wa ma-ring mawili? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Haji Makame Mlenge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunayo changamoto kubwa sana katika vituo vingi vya Polisi, shida kubwa ikiwa usafiri. Yapo maeneo hata ya wilaya nzima kabisa ikiwemo Wilaya ya Kongwa, gari pale ni mbovu na iko moja.

Mheshimiwa Spika, Zanzibar kule vituo hivi viko karibu karibu sana. Katika kugawa magari haya tutaangalia sana hata ukubwa wa jiografia, tutaangalia pia maeneo yenye changamoto kubwa zaidi hasa ya mipakani. Vile vile niseme tu, kwa maeneo ambayo vituo viko karibu karibu, huduma ile wanaweza kuipata katika wilaya, kwa sababu setup yetu katika vituo vya Polisi, bado ni ya kiwilaya zaidi, siyo vituo vile vidogo vidogo. Kwa hiyo, niseme tu tutakwenda kuangalia tuone umbali kati ya kituo hiki anachokisema na kituo cha wilaya halafu tuone kama hilo analolisema litawezekana. Ahsante sana.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kuwa changamoto ya wananchi wa Chwaka inafanana kabisa na ya wananchi wa Jimbo la Mlimba, kwenye Kituo cha Polisi cha Mlimba: Je, Mheshimiwa Waziri haoni hayo magari yatakapofika katika mpango wake, basi aweze kukumbuka pia na Kituo hiki cha Polisi Mlimba? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunafahamu kwamba changamoto hii, kama nilivyosema, iko katika vituo vingi. Naamini hata Kituo cha Polisi cha Mlimba ambacho kina hadhi ya Kituo cha Wilaya kina changamoto kubwa sana ya gari. Kwa kawaida hata angalau magari yakipungua sanakwenye Kituo cha Wilaya, yanapaswa kuwa angalau matatu au manne, lakini pale kuna gari moja na lingine bovu.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo yenye changamoto za miundombinu, changamoto za shughuli za uzalishaji ndiyo zitapewa kipaumbele magari haya yatakapofika.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, kutokana na majibu hayo ya Serikali: Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kutoa ufafanuzi kwa wananchi hao ya tofauti kati ya fidia na kifuta machozi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Je, kutokana na malalamiko ya wananchi hao kuwa mengi, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuongozana nami jimboni ili kwenda kuwasikiliza wananchi hao na hatimaye kutatua matatizo hayo? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE NA URATIBU): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chaurembo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na swali la pili kwamba niko tayari wakati wowote kufuatana na Mheshimiwa Mbunge ili kwenda kuwasikiliza wananchi. Bahati nzuri nilipata fursa ya kukutana na baadhi yao na kwa niaba yangu alikutana nao Mheshimiwa Jafo Dar es Salaam, na tulipokea barua yao na baadhi yao tunaendelea kuwasiliana nao. Tutafanya hivyo ili tukawasilikilize kule kule kwa sababu ndiyo kazi ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni ufafanuzi wa tofauti ya maafa au fidia na kifuta machozi. Maafa yanasababisha na majanga, majanga na huwa si jambo lililopangwa au kutarajiwa, majanga yanaweza kutokana na nguvu za asili, inaweza ikawa na mafuriko, au Tsunami, pia majanga yanaweza yakatokana na matokeo mbalimbali ya nguvu ambazo siyo za kawaida. Inaweza ikawa ni mlipuko wa magonjwa, na yenyewe hayo pia ni majanga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, yanapotokea maafa, huwezi ukayawekea utaratibu wa kulipa fidia. Kwa hiyo, hakuna utaratibu wa fidia kwa majanga, bali ambacho hutokea, jamii au Serikali huweza kutoa kifuta machozi au mkono wa pole kwa walioathirika. Kwa hiyo, Serikali ilifanya hivyo na iliwalipa kifuta machozi. Pia Serikali ililipa kifuta machozi kiasi cha Shilingi 17,464,944,954/=, fedha hizi ni nyingi.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali ilishughulikia mazishi ya wale ambao walifariki katika tukio lile. Naomba kuwasilisha.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningeomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa waombaji wengi wanasifa za kitaaluma za jumla zinazofanana kwa sababu wamesoma katika vyuo au shule za pamoja hapa nchini, lakini bado malalamiko yapo mengi kwa sababu hamna nafasi wanazopata katika ajira katika Wilaya kadhaa.

Je, Serikali sasa iko tayari kutoa orodha za kiwilaya wakati inatoa hizo ajira ili waonekane wale katika kila Wilaya waliopata nafasi?

Swali la pili, kwa kuwa hapa Bungeni Serikali ilisema mwezi wa pili kwamba wale wote sasa ambao wapo kwenye database waliofika katika hatua ya mahojiano au oral watapelekwa kwenye vituo au watapangiwa moja kwa moja katika vituo, lakini practice kwa sasa inaonesha si hivyo, kuna watu wanachomekwa chomekwa.

Je, Serikali iko tayari kutoa orodha ile ambayo iko kwenye database ili wananchi waweze kuona wanaopangiwa kwamba ni wale ambao wako kwenye orodha? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA N AUTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba waombaji wengi wana sifa zinazofanana na kwa kweli wamesoma kwenye vyuo vyetu lakini changamoto tunayoipata hapa ni kwamba pamoja na sifa hizo lakini nafasi ni chache, kwa hivyo namna pekee ya kuweza kuwapata hawa wanaotakiwa, mathalani nafasi zinaweza zikatangazwa labda 200, waombaji wakawa 1,000, namna pekee ya kuwapata hawa 200 ni lazima tu uwashindanishe. Sasa huo ushindani haumaanishi kwamba pengine wengine walisoma ni bora zaidi, ni kama mbio tu za marathon, lakini kimsingi tungetamani wote wanaoomba wapate lakini nafasi ni chache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kutoa orodha au kuweka utaratibu wa mfumo wa kiwilaya na wenyewe bado tunaendelea kuutafakari kama nilivyosema kwenye majibu yangu wakati tunahitimisha bajeti yetu kwamba tutajitahidi ku – design mfumo ambao utawabaini waombaji na maeneo wanayotoka ili tuweze kutafuta hicho ambacho kilisemwa sana kwa sauti kubwa na Waheshimiwa Wabunge juu ya hisia za upendeleo wa kimaeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili tunaendelea kulifanyia kazi na mpaka sasa tumeunda timu inajaribu kuchakata tuone namna gani bora siyo jambo jepesi, ukilisema hivi kama jepesi lakini kiuhalisia ni ngumu kutengeneza mfumo utakaobaini maana yake hatufuati kabila. Kwa sababu mwingine anatokea mahala kulingana na asili alikokulia au anaomba akiwa yuko Dar es Salaam hatokei Kibakwe lakini anaomba yuko sehemu nyingine, je unamuwekaje? sasa hilo nalo tunaendelea kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwamba wale waliokwishafanya usaili na mfumo wetu wa usaili ni wa aina mbili, kwanza ni wa kuandika na mwingine ni usaili wa kuulizwa maswali ya papo kwa papo. Sasa wanapotokea watu wamefika kwenye hatua ya pili maana yake wamejitahidi kufanya vizuri na pale napo utampata wa kwanza mpaka wa mwisho lakini uhitaji pengine ni wachache wanaobaki ndiyo Mheshimiwa Mbunge anasema kuwepo na uwazi ili wajulikane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie kwamba tutajitahidi sana kuweka uwazi huo ili wajulikane, ili wanapochukuliwa wao wenyewe wadhihirishe kwamba kweli alikuwa wa kadhaa na waliochukuliwa na yeye ameweza kupata fursa ili tuondoe haya manung’uniko.
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa nchi yetu kwa sasa ina wahitimu kila kona, na kwa sasa kwa sababu mfumo ulioko wa kuomba ajira una changamoto na una manung’uniko mengi.

Je, Serikali iko tayari sasa kupitia mfumo huu wa sasa ili kupeleka kwenye kila Jimbo idadi sawa ambayo itakwenda kutibu sasa tatizo hili la manung’uniko ambalo kwa kweli kila kona lipo? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA N AUTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili halitofautiani nalile lililoulizwa na Mheshimiwa Mtemvu, tofauti ni kwamba Mheshimiwa Mtemvu kasema Wilaya lakini Mheshimiwa Mbunge kasema Jimbo. Kama nilivyosema tunaendelea kufanya utafiti kwa kutumia mifumo lakini na uhalisia wa jambo lenyewe kama tunaweza tukalitekeleza katika usahihi sana kinyume na utaratibu wa sasa wa kushindanisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna upungufu kwenye kushindanisha au kama hakuna uwazi wa kutosha kwenye kushindanisha inaweza ikawa kazi nyepesi zaidi kushughulikia kuliko kutafuta mfumo utakaoweza kuja na majawabu haya. Hata hivyo, katika jibu langu la msingi nimesema kwamba tutajitahidi kuandaa, tumeunda timu ambayo inaendelea kufanya utafiti hata sasa wako kazini watatuletea majawabu ya namna gani tunaweza kufanya yote mawili mfumo na uhalisia ili tuweze kuona manung’uniko haya yanakwisha kabisa. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Mimi nimemsilikiza sana Mheshimiwa Waziri na nimemuelewa lakini nataka niiambie Serikali kwamba akina Simbachawene kule Sikonge wako wengi tu na akina Lusinde na wakina Mpangala. Kwa hiyo, suala siyo kabila au asili ya mtu, suala ni anuani. Kwa nini anuani zile zisitumike kuweka wazi kwamba huyu anuani yake ni P.O.Box 8 – Sikonge, ukawa na watu labda 20 ambao umewaajiri kutoka Sikonge ukaonesha pale, kwa nini isiwe rahisi namna hiyo badala ya anavyofikiria ukabila na mambo mengine? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA N AUTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema kwenye jibu langu la msingi, nataka aniseme tu Mheshimiwa Kakunda alichokisema ni kwamba tuende kwenye anuani. Tukienda kwenye anuani pia kuna confusion bado, bado utaiona tu confusion kwa sababu utaichukua anuani, unataka kumchukua mtu aliyetoka kwenye Jimbo anakotoka Mheshimiwa Kakunda, lakini utatumia chuo alichosoma, utatumia mahali alikokulia, utatumia anuani alikoombea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, so kuna mambo mengi ya kuyaangalia ndiyo maana tunasema huo mfumo tunaouangalia na ushahidi tunaoungojea wa kitaalamu na utafiti unaofanyika utatusaidia zaidi kuliko hapa sasa hivi nikisema tutafata utaratibu huu. Nadhani mtuachie Serikali tulifanyie kazi tunaweza tukaja na kitu kizuri zaidi. (Makofi)
MHE. RASHID ABDALLA RASHID: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba uhakiki umefanyika na wananchi hao wamesharejeshwa, lakini ni lini sasa watapatiwa malimbikizo yao ya ruzuku kutoka pale ambapo walisimamishwa na ukizingatia kwamba hasa hawa ambao walisimamishwa ni wanawake?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna makundi mawili; la kwanza ni wale ambao baada ya uhakiki walionekana wamekosa sifa na hawa ni 2,500 lakini wako ambao walipokosa sifa walikata rufaa wakarejeshwa, tutaangalia uwezekano wa kuanzia pale walipokuwa wamesimama au taratibu zinatakaje ili waweze kulipwa au wataendelea kuanzia hapa ambapo wamekuwa cleared.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili ni jambo la kulifanyia kazi, tutawasiliana na Mheshimiwa Mbunge muuliza swali Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi ili atuambie hasa ni wapi, lakini kimsingi Serikali ili wapembua kwa makundi hayo mawili na uamuzi huo ndio ulikuwa umefikiwa mpaka hatua za mwisho.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kati ya waliopata sifa ni pamoja na wanawake na kaya nyinginezo za Mkoa wa Kilimanjaro ambao walipewa sasa ajira za muda, lakini baada ya kufanya ajira hizo vizuri hawajalipwa kwa vipindi viwili sasa.

Je, ni lini, Serikali itatoa malipo hayo ili malalamiko yaondoke katika mioyo yao?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyomgeza la Mheshimiwa Shally Raymond kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii ni taarifa na nimeisikia sasa kutoka kwake kwamba Mkoa wa Kilimanjarpo kuna wale ambao waliofanya kazi za TASAF za miradi ya kipindi maalumu na kwamba bado hawajalipwa basi acha tukalifanyie kazi halafu tutawasiliana na Mheshimiwa Mbunge.