Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Joseph Kizito Mhagama (53 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nimshukuru sana Mwenyenzi Mungu aliyenijalia wakati huu kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia kwa unyenyekevu mkubwa sana niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Madaba ambao kwa umoja wao wamenituma nifanye kazi yao wakiamini kwamba nitawatendea haki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kupongeza sana hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa kwa Bunge lako Tukufu. Hotuba hii imejaa hekima kubwa lakini pia imejaa matumaini makubwa sana kwa wananchi wa Tanzania na hasa kwa wananchi wa Jimbo langu la Madaba. Hotuba ya Mheshimiwa Rais kwa sehemu kubwa imetoa mwelekeo wa Taifa letu kwa kipindi cha miaka mitano. Kwa hakika hotuba yake imeshakwishaanza kutafsiriwa kwa vitendo kupitia utekelezaji wa kazi hizo, lakini pia kwa kupitia Baraza lake la Mawaziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Mawaziri wote wa Awamu ya Tano, wanafanya kazi kubwa kwa ajili ya Watanzania. Kwa namna ya pekee sana naomba sana niwashukuru sana Mawaziri ambao tayari wameshakuja kwenye Jimbo langu na tayari wameanza kufanya kazi na wananchi wa Jimbo langu. Kwa namna ya pekee nimshukuru Mheshimiwa Ummy Mwalimu, tayari amekuja kuangalia changamoto za afya na sasa yupo kwenye mchakato wa kuhakikisha kwamba tunapata hospitali ya Wilaya, tunamshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa heshima kubwa nimshukuru sana Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo, Waziri wa Nishati na Madini katika mazingira magumu na muda mgumu alifika katika Jimbo langu kuangalia changamoto ya umeme na kuipatia majibu pale pale. Namshukuru na kumpongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika uchangiaji wangu nitajikita katika maeneo machache muhimu yanayohusu maslahi ya Taifa letu. Moja ni eneo la viwanda. Katika hotuba ya Mheshimiwa Rais toka ukurasa wa 13 – 16 anaeleza ni namna gani Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kuifanya sekta ya viwanda iwe sekta mama itakayotoa ajira za uhakika kwa Watanzania. Mheshimiwa Rais anakwenda mbali zaidi na kueleza namna gani hiyo sekta ya viwanda inakwenda kujibu matatizo ya masoko ya mazao, mifugo pamoja na uvuvi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii kwa uzito ambao Mheshimiwa Rais ameupa na kwa hali halisi ya Tanzania ni sekta muhimu sana. Nitumie nafasi hii kupongeza hatua ya Mheshimiwa Rais kuzingatia viwanda lakini naomba nitoe tahadhari kwa wale ambao wamepewa kusimamia utekelezaji wa jukumu hili. Moja, lazima tujue kwamba sekta ya viwanda ina mahusiano makubwa sana na sekta ya biashara lakini pia kwa sababu hivyo viwanda vinahusu kilimo, uvuvi na mifugo, sekta hizi zote zinafanya kazi kwa karibu sana. Sera ya kuimarisha viwanda ndani ya Tanzania siyo sera ngeni, kigeni katika Awamu hii ya Tano ni mikakati mipya ambayo Mheshimiwa Rais amekuja nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tujifunze ni nini kilisababisha viwanda vyetu vya miaka ya 1980 na 1990 na kuelekea mwaka 2000 vikafa. Mikakati ya ndani ni mizuri, mitaji ilipelekwa lakini naomba wanaohusika na maandalizi na usimamizi wa eneo hili wakubali kurudi tena kwenye kusoma uzoefu hasa unaogusa sera zetu za nje, mikataba yetu na makubaliano ya kibiashara na mataifa mbalimbali zikiwemo jumuiya mbalimbali zenye maslahi ya kibiashara na Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukifuatilia kwa undani pamoja na jitihada za ndani za kuzalisha mazao ya viwandani, mazao yetu yameendelea kukosa soko kwa sababu tumefungulia kiholela mazao ya viwandani yanayotoka mataifa mengine. Ndani ya Mkoa wa Ruvuma nimepambana sana kwa miaka zaidi ya sita kuhakikisha kwamba sekta ya mazao ya mafuta yakiwemo alizeti inakuwa sekta tegemezi kwa uchumi wa Mkoa wa Ruvuma kwa kuhakikisha kwamba tunazalisha mafuta ya kula ya kutosha yatakayoweza kukidhi mahitaji ya mkoa. Hata hivyo, jitihada hizo zimeangamizwa na mafuta ya bei rahisi yanayoingizwa toka Malaysia na nchi nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hilo eneo halitaangaliwa vizuri, Watanzania tutaenda kuwekeza kwenye viwanda na tutafilisika na tutabaki maskini wa kutupwa kwa sababu Tanzania mpaka sasa imeendelea kuwa soko kubwa la mazao ya viwandani yanayotoka nchi zingine. Kwa hiyo, nashauri sera yetu inayohusiana na maeneo hayo iangaliwe vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ni mama kwa uchumi wetu ni kilimo na mifugo. Niishukuru sana Wizara ya Kilimo, Mheshimiwa Waziri Mwigulu na timu yake wananchi wa Madaba kwa namna fulani wamefaidika sana na Wizara hii kwa asilimia 75 ya wakazi wake kufanikiwa kupata pembejeo za ruzuku.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu wa ruzuku siyo endelevu. Msimu wa mwaka jana wananchi wa maeneo yale hawakupata pembejeo za ruzuku iliathiri sana uzalishaji wao. Najua mfumo huu umechukua uzoefu kutoka Malawi na maeneo mengine na hapa tunau-apply. Naomba Wizara inayohusika na kilimo na mifugo tuchukue hatua za makusudi kujifunza mifumo mingine inayopendekezwa na wadau mbalimbali wa kilimo. Najua kumekuwa na miradi mbalimbali ya wadau wa kilimo inayojaribu mifumo mbalimbali ya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata pembejeo kwa namna endelevu. Naomba sana Wizara hii iandae utaratibu maalum wa kufanya utafiti wa mifumo inayofaa. Mfumo huu hauna uendelevu kwa sababu unategemea asilimia 100 ruzuku ya Serikali, ruzuku ambayo hatuna uhakika nayo. Kuna mifumo ya kuwaunganisha wasindikaji, wanunuzi wa mazao, wasambazaji pembejeo pamoja na vikundi vya wakulima kwa kupitia mfumo wa mikataba ambayo itawasaidia kupata mikopo ya pembejeo, uhakika wa masoko ya kilimo na uhakika wa uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo mengi nyeti yanayowagusa wananchi wa Jimbo la Madaba, eneo la soko la mazao ni mgogoro sana kwa sababu mpaka sasa tunategemea Serikali pekee kununua mahindi kupitia NFRA. Nashukuru sana Wizara ya Kilimo wamefanya jitihada kubwa sana kukarabati maghala ya kuhifadhia mazao wakati wa mavuno. Hata hivyo, maghala yale yametengenezwa kwa pesa za wakandarasi, wakandarasi hawajalipwa, hawajamaliza na mwezi wa sita wananchi wanaanza kuvuna hawana mahali pa kuhifadhia mazao yao, tunaomba hilo nalo liangaliwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo gumu sana kwetu Madaba ni maji. Wananchi wa Madaba hawana maji, Jimbo la Madaba ni jipya, Halmashauri ya Wilaya mpya, Makao Makuu maji ni mgogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nikushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Mpango huu wa Miaka Mitano unaeleweka vizuri iwapo utasomwa katika context yake ya kwamba Mpango huu unatokana na Mpango Elekezi wa Miaka 15. Ukishauweka katika context ya miaka 15 unaelewa kwamba kilicholetwa hapa kwa miaka hii mitano ni hatua ya pili ya utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Miaka 15. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukishaelewa hivyo, unaweza ukapunguza sana kejeli ambazo zinatolewa na baadhi ya Wabunge humu ndani. Hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mradi huu ilikuwa kutanzua vikwazo vya uchumi; ni hatua nzuri ambayo imefikiwa kwa kipindi cha miaka mitano tunachokimaliza msimu huu wa 2015/2016.
Mheshimiwa Spika, tunapokuja na Mpango wa miaka mitano inayoanzia mwaka 2016/2017, tunazingatia pia uzoefu tulioupata miaka mitano iliyotangulia. Ukiangalia katika Mpango huu, miaka mitano iliyopita ilieleza bayana, pamoja na kutanzua vikwazo vya uchumi, pia kipindi hicho cha miaka mitano iliyotangulia kilienda sambamba na kubaini maeneo ya vipaumbele. Maeneo ya vipaumbele yaliyobainishwa ni pamoja na Miundombinu, Kilimo, Viwanda, Rasilimali Watu, Huduma za Kifedha, Utalii na Biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunapotoka kwenye awamu ya kwanza na tunapokwenda kwenye awamu ya pili ambayo itachukua tena miaka mitano, tumechagua eneo la viwanda kama eneo mahususi la kulifanyia kazi. Mpango huu ukiusoma kwa umakini na ukaulewa, utaelewa ni kwa nini sasa tumechukua viwanda na kwa nini Mpango huu umeitwa kama kipaumbele kujenga misingi ya uchumi wa viwanda? Tunapoongelea viwanda, tunaenda sambamba na miundombinu ambayo itafanya viwanda viimarike lakini biashara iimarike. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mpango huu umebainisha vizuri maeneo ya ujenzi wa barabara, reli, bandari, lakini pia umeeleza miradi mahususi ambayo itaifanya Tanzania yetu iwe Tanzania mpya, Tanzania ambayo inakwenda kujibu kero za vijana, akinababa na akinamama wa Taifa hili. Ukiusoma katika context hiyo, unakubaliana nami kwamba Mpango huu wa miaka mitano kama sehemu ya utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Miaka 15, Mpango huu umekaa vizuri kwenda kutatua matatizo ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Serikali nzima ya Awamu ya Tano kwa kujifunza kutokana na uzoefu wa miaka mitano iliyotangulia na kuja na Mpango madhubuti utakaolijenga Taifa letu vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninavyouangalia Mpango huu na namna ulivyokaa, nina maeneo machache ambayo ningependa nishauri. Ukiangalia Mkoa wa Ruvuma ambao lango lake lipo katika Jimbo ninaloliongoza, Jimbo la Madaba unaona kwamba Mkoa wa Ruvuma umejaa fursa nyingi sana ambazo kama zitatumiwa vizuri na Mpango huu, kwa hakika Tanzania itakuwa nchi ya neema sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, zipo barabara muhimu ambazo zitatakiwa zijengwe na ziimarishwe ili Mpango huu wa viwanda uweze kuwanufaisha wananchi wa Jimbo la Madaba na wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla ambao kwa asilimia kubwa wanachangia sana pato la Taifa na wanachangia sana chakula kinacholisha Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, Jimbo langu la Madaba linapakana na Wilaya ya Ulanga, lakini kufika Wilaya ya Ulanga nahitaji kufika mpaka Mikumi na baadaye niende Ifakara ndipo niende Ulanga. Wakati wananchi wangu wa Kijiji cha Matumbi wanatumia siku sita kwa mguu au nne kufika katika Wilaya ya ulanga, lakini wanatumia siku mbili kwa mguu kufika mpakani mwa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba na upande wa pili wa Malinyi.
Mheshimiwa Spika, hicho tayari ni kikwazo kikubwa sana cha uchumi kwa maendeleo ya maeneo yote mawili. Pamoja na kwamba Mpango huu bado haujabainisha nini kitafanyika, haujafafanua, nafikiri kwa sababu Mpango huu una sifa ya kujifunza kwa Mipango iliyotangulia, basi tuendelee kuangalia lile eneo ambalo linapakana na Jimbo la Madaba kama sehemu moja muhimu ambayo itachangia sana uchumi wa wananchi wa maeneo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia imeelezwa vizuri sana kwamba Mkoa wa Lindi unapakana na Mkoa wa Ruvuma, nalo ni eneo muhimu sana kama tunataka kuimarisha uchumi wa wananchi wale kupitia viwanda kwa sababu tunazalisha malighafi ya kutosha, tunahitaji kusafirisha, lakini tutazalisha bidhaa nyingi za viwandani, tutahitaji ziende Lindi, Ifakara, Mahenge na maeneo mengine ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa miaka mingi sana Mbunge aliyemtangulia Waziri Mheshimiwa Jenista Mhagama, Mbunge Profesa Simon Mbilinyi, aliyestaafu, alianza kuongea sana kuhusu miradi ya NDC, hususan mradi wa Mchuchuma na Liganga. Mheshimiwa Waziri Jenista Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Peramiho, ambaye sasa kipande cha Jimbo lile kimekuwa Jimbo la Madaba, ninaloliongoza sasa, kwa miaka kumi amesimamia ajenda hiyo ya mradi wa Mchuchuma na Liganga.
Mheshimiwa Spika, mradi ule kama utafanikiwa kwa kiwango hiki ambacho umeelezwa katika Mpango huu, kwa hakika utatukomboa sana wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, utawakomboa sana wananchi wa Madaba na Jimbo la Peramiho. (Makofi)
Mheshimwa Spika, ni vizuri sasa, kwa vile maandalizi ya kuanza ku-explore ule mradi wa Liganga Mchuchuma, ni vyema sasa barabara inayotoka Wilaya ya Ludewa kufika Madaba iimarishwe ili kwamba wananchi wa pale waweze kunufaika na ule uchumi, lakini pia ndiyo barabara inayokuja kuunganisha na barabara ya Makambako kuja Dar es Salaam, kwa ajili ya kusafirisha mali na bidhaa zitakazozalishwa katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, tuna usemi wa Kiswahili, Waswahili wanasema, “Siku ya kufa nyani, miti inateleza.” Wakati nipo nje ya Bunge hili, kuna wakati nilikuwa naona kuna baadhi ya hoja zenye mashiko kutoka upande wa pili wa upande wangu wa kulia, lakini kadri ninavyozidi kukaa ndani ya Bunge hili, katika hiki kipindi cha miezi kama sita hivi nimekaa hapa, nazidi kuona kwamba hoja zenye mashiko zinazidi kupungua. Naamini sasa kweli miti inateleza. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna wakati ambapo hoja ya ufisadi ndiyo ilikuwa mhimili mkubwa wa kushikilia. Leo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa John Pombe Magufuli alipoisimamia hoja ya kutumbua majipu na kuondoa mafisadi, wale wale ambao walikuwa wameshikilia hiyo nguzo, wanamlalamikia na wanamlaumu. Ama kweli Waheshimiwa Wabunge ni lazima tujipime wakati mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, inanisikitisha sana ninapoona mtu anaji-contradict mwanzo hadi mwisho wa hotuba yake. Anaanza na kusema Baraza la Mawaziri halifanyi kazi, halifai. Baraza hili ni lile lile la Awamu ya Nne, wanabadilishana nafasi, halafu baadaye anasema Mheshimiwa Waziri fulani umenifaa sana, unafanya sana kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuishi kwa contradiction. Lazima tuwe na consistent katika hoja zetu. Leo nimependa sana…
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, lazima ni-declare interest, approach aliyoitumia Mheshimiwa Ally Saleh, imetujenga sana na imemsaidia sana Waziri wa Fedha kuweza kuboresha Mpango huu wa Miaka mitano wa Maendeleo. Napenda sana tutumie approach hiyo ili kuisaidia nchi yetu na kuwasaidia Mawaziri waweze kutuletea majibu yanayostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunalo eneo lingine muhimu sana kwa Jimbo la Madaba…
TAARIFA
MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa kanuni ya 68 (8)!
SPIKA: Mheshimiwa Joseph, naona kuna taarifa ambayo haivumiliki...
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika ahsante. Taarifa hiyo siipokei kwa sababu wale ambao walileta ushahidi ndani ya Bunge hili, mimi nikiwa nje ya Bunge hili, kwamba Mheshimiwa Lowassa ni mmoja katika mafisadi wakubwa, ndio hao hao waliomkumbatia na kwenda naye katika kampeni ya Awamu hii ya Tano. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)
MBUNGE FULANI: Wanafiki wakubwa!
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, kwa namna yoyote siwezi kuipokea hiyo taarifa. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha
kwa muda wa mzungumzaji)
SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mhagama, muda wako umekwisha. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya TAMISEMI kukushukuru wewe, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wa Bunge ambao wametupa ushirikiano mkubwa sana kama Kamati. Nitumie pia fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote pamoja na Naibu Mawaziri ambao wamepata fursa yakuchangia taarifa hizi zote mbili ambazo zilikuja mbele yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee niwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliyochangia hoja za Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria ambao kwa idadi yao wanafikia sita pamoja na Naibu Mawaziri watatu, walichangia hizi hoja kwa ufasaha sana na Waheshimiwa Wabunge na Naibu Mawaziri wote waliyochangia walipata fursa ya kuunga mkono maeneo yote ambayo kamati yetu ilileta kama mapendekezo kwenye Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo kadhaa ambayo nilitamani niwekee mkazo kwa sababu kwa sehemu kubwa michango yote ya Wabunge na Naibu Mawaziri imejielekeza kuunga mkono hoja pia kulihitajika ufafanuzi kwa baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hoja zetu za Kamati, Kamati ilipendekeza kwa Serikali, iliitaka Serikali kupitia Wakala wa Ndege za Serikali kuongeza ndege moja kwa ajili ya matumizi ya viongozi. Ipo kasumba kwa baadhi ya Watanzania wenzetu kuamini kwamba kila aina ya usafiri ni starehe lakini wewe unajua uwekezaji kwenye vyombo vya usafiri siyo wakati wote ni starehe na vyombo vya usafiri siyo wakati wote ni liability, wakati mwingine au kwa sehemu kubwa usafiri unaohusu masuala ya utawala ni asset.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana na mimi ndege ya Serikali F28, ilinunuliwa mwaka 1978 na ilinunuliwa na Baba wa Taifa kwa matumizi ya Serikali kwa maana ya viongozi, in aumri sasa wa zaidi ya miaka 39 bado watu wanaamini kwamba tungeweza kutumia fedha hizi tunazopendekeza kujenga vituo vya afya na zahanati, lakini ili haya yote yaweze kufanyika ni lazima kuhakikisha kwamba viongozi wetu kwanza wanakuwa salama lakini pili wanasafiri kwa haraka ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kujenga nchi kubwa kama Tanzania bila kuhakikisha kwamba wale viongozi wakubwa ambao tunawakabidhi majukumu mazito yakusimamia maslahi mapana ya Taifa letu hawawekewi mazingira salama ya usafiri lakini mazingira yatakayo wawezesha kufanya kazi hizo kwa ufanisi mkubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya awamu ya sita kwa haraka haraka tu imejenga hospitali za Kanda 16, imejenga hospitali za Mikoa 62, imejenga hospitali za Wilaya 351 lakini tunavyo vituo vya afya 1,126, tuna idadi ya zahanati zaidi ya 7,000, tuna shule za sekondari zaidi ya 486. Haya yote yamefanyika ndani ya Awamu hii ya Sita, mambo haya yanahitaji uwezeshwaji mkubwa wa shughuli za kiutawala, kuwawezesha viongozi wetu kuweza kuendelea kuyasimamia haya yaliyokwisha fanikiwa lakini kwenda kuwezesha mengine mengi zaidi ambayo Watanzania tunayahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niliombe Bunge lako liridhie Maazimio haya ya Kamati ya kuitaka Serikali iongeze ndege moja kwa ajili ya kuwezesha shughuli za utawala kwa matumizi ya viongozi ili F28 iweze kupumzishwa ili kurinda usalama na ustawi wa viongozi wetu ambao wanafanya kazi kubwa sana kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ambayo nilitamani niifafanue na niiseme kidogo kwa kina ni hoja hii ya madawa ya kulevya. Madawa ya kulevya ni janga kubwa sana kwa Taifa letu, hii nashukuru Waheshimiwa Wabunge waliyopata nafasi ya kuchangia wamesema hivyo akiwemo Mheshimiwa Florent Kyombo - Makamu Mwenyekiti wa Kamati hii lakini pia Mheshimiwa Naibu Waziri Patrobass Katambi, ameelezea kuhusu hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha ukisikiliza takwimu. Kati ya mwaka 2017 mpaka 2020 matumizi ya madawa ya kulevya yameongezeka mara nne, yameongezeka mara nne katika muda huo mfupi lakini idadi ya watumiaji wa madawa ya kulevya kwa takwimu za mwaka 2019 duniani walifikia milioni 200. Sasa milioni 200 tafsiri yake ni nini, hii kwanza ni asilimia nne ya watu wote waliopo duniani na tafsiri yake nini, tafsiri yake katika kila watu 100 watu wanne wanatumia madawa ya kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge hapa tupo karibu mia tatu na tisini na kitu, tafsiri yake ni nne mara nne kama watu 16 watakuwa wanatumia madawa ya kulevya. Naeleza tu tafsiri ya kitakwimu, hizi ni tafsiri za kitakwimu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hali hii siyo ya kuifanyia dhihaka, niweke tu taarifa vizuri kwamba huu ni mfano kwamba tuna Wabunge karibu 400 humu ndani na kwa tafsiri ya nne kwa 100 maana yake ni kama watu 16 siyo jambo la kulifanyia dhihaka na wote tunajua madhara ya matumizi ya madawa ya kulevya, Taifa letu linaangamia, Watanzania wanazidi kuwa useless katika sekta ya ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya ukifuatilia hata wale wanaopata huduma za urahibu wapo pia watumishi wa umma ambao wameonekana wanatumia haya madawa ya kulevya, kwa hiyo hatari yake ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nilitaka niliombe Bunge lako tumpongeze sana, sana Kamishina Jenerali Arestas James Lyimo ambaye ameonyesha mfano katika usimamizi wa jambo hili, lakini niipongeze sana Serikali katika ujumla wake wamefanya kazi kubwa sana kwenye usimamizi na udhibiti wa matumizi ya dawa za kulevya pamoja na biashara yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuja na mapendekezo mahsusi au pendekezo mahsusi kwenye eneo hili na misingi ya pendekezo letu ni hii. Mnafahamu kwenye taarifa yetu mmeona yapo mashauri 1,158 ya dawa za kulevya hadi sasa, kati ya hayo ni mashauri 64 pekee ndiyo yamefanyiwa kazi hadi sasa. Kwa hiyo, mnaweza mkaelewa mzigo mkubwa ambao Mahakama zetu zinazo. Kwa hiyo, tumetoa ushauri, tumetaka iundwe division maalum ambayo itakuwa inashughulikia mashauri ya madawa ya kulevya, faida zake ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza itawawezesha watoa maamuzi kwa maana ya Mahakimu wetu kubobea kwenye eneo hili la madawa ya kulevya mbinu na mikakati ambayo inatumiwa na wahalifu kwenye eneo hili, pia itawezesha Serikali kutenga rasilimali mahsusi kabisa kwa kushughulikia mashauri ya aina hii ili yaishe kwa wakati ili Watanzania wawe salama zaidi. Nashukuru katika michango ya Waheshimiwa Wabunge hakuna ambaye ameonesha kutoridhika na hoja hii na ninaamini Bunge lako litaipitisha kwa maslahi mapana ya Watanzania lakini kwa usalama wa Taifa letu na watoto wetu. Hayo ni maeneo mawili muhimu ambayo nilitaka niyaseme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge pia wameongelea kuhusu Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kwenye hili niseme tu kifupi kwa sababu muda umeisha, Serikali mnakumbuka tumelizungumza sana suala hili. Watanzania wengi wanalalamika juu ya haki zao kuvunjwa na kwa sehemu kubwa zinavunjwa na baadhi ya taasisi ambazo tumezitungia sheria ya kusimamia mambo mbalimbali. Kwa hiyo, tunaomba sana hizi sekta za taasisi za umma ambazo zimepewa wajibu wa kuwahudumia Watanzania kwa namna moja au nyingine wahakikishe wanalinda haki za binadamu na wanasimamia utawala bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora tumeielekeza ilete taarifa mbele ya Kamati na hapa niombe kusisitiza kwamba tupewe hii taarifa ya Tume ili Kamati ipate mwanya au fursa pana yakuishauri Serikali juu ya malalamiko mengi ambayo Watanzania wanayo juu ya uvunjifu wa haki za binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo mengine ambayo yamekwisha zungumzwa, masuala ya Muungano mnajua credit kubwa inaenda kwa Mheshimiwa Rais mwenyewe kuhakikisha kwamba hoja 22 kati ya hoja 25 zinafanyiwa kazi na taasisi 33 kati ya taasisi 36 za Muungano ambazo zilitakiwa ziwe na ofisi Zanzibar, tayari zinaofisi, hayo ni mafanikio makubwa na hii ni credit kubwa kwa Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua tunayo Sheria ya Maafa, tumeona namna ambavyo Serikali imeshughulikia maafa na Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa, nami niseme tayari tunayo sheria ya kushugulikia maafa nchini, ina miaka kama mitatu hivi, lakini tumetengeneza mfuko kisheria wa kushughulikia maafa nchini. Tunao mkakati mahsusi wa kushughulikia maafa nchini. Kamati imeomba taarifa juu ya utekelezaji wa haya yote ninaamini Serikali itajipanga ilete mbele ya Kamati taarifa hizi ili pia iweze kushauri na ilete mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho lilikuwa msaada wa kisheria kwa kupitia hii Mama Samia Legal Aid. Tunajua namna ambavyo imekuwa na faida kubwa kwa Watanzania na hapa imetolewa mifano kivipi leo Watanzania kwa idadi kubwa ile wanakwenda kueleza matatizo yao kwa viongozi wetu wa chama. Ni jambo zuri ni kwamba watanzania wana imani na Chama Cha Mapinduzi, wana imani na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni taswira nzuri lakini nyuma yake kuna changamoto. Changamoto mojawapo ni kwamba hawa wananchi wetu wengi hawajapata nafasi yakusikilizwa, kwa hiyo moja ya namna nzuri ya kutatua changamoto hii ni kuiwezesha Mama Samia Legal Aid iweze kufikisha huduma kwa Watanzania walioko vijijini. Kwa hiyo Serikali inapotafakari namna yakutatua changamoto hizi pamoja na zile ambazo Waheshimiwa Wabunge wamesema, iangalie uwezekano wa kuongeza nguvu kwa Mama Samia Legal Aid iweze kuwafikia Watanzania wengi zaidi waweze kupata suluhu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza Naibu Waziri wa masuala kwa sasa yupo ardhi lakini alikuwa Katiba na Sheria huko nyuma, ameeleza kwamba hatuwezi tukawatumia Maafisa wa Sheria wa Halmashauri kwenye eneo hili lakini sasa ndiyo hatuna watu tufanyeye, Serikali mtupe suluhisho kwenye jambo hili ili tuweze kukabiliana nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba nitoe hoja ya kwamba tunaliomba sasa Bunge lako Tukufu liridhie hoja za Kamati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. DKT. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge waliochangia jana kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais pamoja na mawaziri wote wawili ambao wamewasilisha mpango wao. Lakini pia nitumie fursa hii kukupongeza wewe na Kamati yako ya Bajeti kwa kazi nzuri ya uchambuzi ambayo mmeifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maslahi ya muda sitaweka utangulizi mrefu, lakini nitajikita kwenye hoja moja ambayo ninadhani ni muhimu sana kwa maslahi mapana ya Taifa letu, ili tuweze kupata ile picha kubwa ya Tanzania tunayoitaka katika kipindi cha miaka mitano, miaka 15, miaka 25, miaka 50, kadiri ya malengo makubwa ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Muda Mrefu. Miongoni mwa vitu ambavyo vimejitokeza kwenye tathmini ya mwenendo wa uchumi wa Taifa letu ni ukubwa wa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa na huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hii umeionesha kwanza kwenye ripoti yako, ukurasa wa sita, umeichambua vizuri sana, ninakupongeza. Lakini pia Mheshimiwa Waziri ameichambua na kuieleza vizuri sana kwenye hotuba yake, ukurasa wa 20. Kwamba, moja katika changamoto ambazo zinatukwamisha sana ni hii nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa na huduma ambayo kwa sehemu kubwa ndio imechangia hata kuadimika kwa dola, lakini pia imekwamisha ufanyaji biashara. Wafanyabiashara wengi wakubwa leo wanashindwa kuagiza bidhaa nje ya nchi kwa sababu hawana Dola. Na hili ni tatizo kubwa sana kiuchumi na hatuwezi kulichukulia katika uzito mwepesi, ni lazima tulichukulie katika uzito wake mkubwa. Ninakushukuru Mheshimiwa Waziri, Profesa wangu, Mheshimiwa Profesa Mkumbo, umelifafanua kwenye ukurasa wa 20 wa hotuba yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa sita wa kamati unaeleza namna ukubwa wa tatizo hili; inaeleza kwamba, kati ya mwaka 2021 na 2022 nakisi imeongezeka kwa asilimia 54.8; hili ni ongezeko kubwa sana. Kamati kwenye taarifa yake inaeleza sababu, Mheshimiwa Waziri hajazisema, lakini Kamati imeeleza sababu za ukubwa wa nakisi hiyo ambayo ina madhara makubwa sana kiuchumi. Nitazitaja zile sababu ambazo ziko ndani ya uwezo wetu kwa sababu, nyingine ziko nje ya uwezo wetu na mimi sipendi kushughulika na mambo ambayo hatuna uwezonayo. Masuala ya vita ya Urusi na Ukraine hayatuhusu, hatuna uwezo nayo, nitazungumza sababu ambazo Kamati imezieleza zile ambazo tuna uwezonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni uagizaji wa bidhaa nyingi za ujenzi kutoka nje ya nchi. Hilo tunalijua, tunajenga SGR, tunajenga miradi mikubwa ya umeme, Bwawa la Mwalimu Nyerere, hayo yamechangia kwa asilimia kubwa sana kuongeza ukubwa wa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa na huduma katika uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiachana na hayo ambayo hatuna uwezo wa kuya-control, kwa sababu tuna miradi hii mikubwa tunaijenga, tunazo bidhaa nyingi ambazo tunaziagiza kutoka nje ambazo zimechangia pia ukubwa wa nakisi hiyo. Moja wamesema mbolea, mbili wamesema mafuta ya kula, tatu wamesema ngano, nne wamesema mazao ya petroli. Kwa hiyo, hayo kwa sehemu kubwa yamechangia ukubwa wa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yaliyotolewa; mapendekezo haya yapo kwenye ukurasa huohuo wa 20 wa Serikali. Wamesema suluhisho ambalo limependekezwa ni kwamba, kupunguza nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa kwa kuongeza mauzo ya nje ya nchi. Yaani tumalize hilo tatizo kwa kuongeza mauzo nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, it is very logical, ni sahihi kabisa, tuongeze mauzo ya bidhaa nje ya nchi ili tuka-attract dola ije, ili tupunguze hiyo nakisi, na ikiwezekana kuiondoa kabisa. Hata hivyo, changamoto yangu ni mapendekezo ya aina ya bidhaa ambazo tunataka tuzipeleke nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo matatu ninakubaliananayo vizuri kabisa. Mheshimiwa Waziri ameeleza kuhusu madini, tunaweza kufanya vizuri tukauza madini sana nje ya nchi. Ameongea kuhusu mazao ya misitu, excellent, tuna uwezo nayo hayo mazao ya misitu, tukayauza nje, tumefanya vizuri. Lakini pia kwenye eneo la huduma ameeleza umuhimu w kupanua huduma ya utalii. Excellent, tutafaulu sana kwenye eneo hilo na tayari tupo vizuri tunaongeza nguvu tu hapo, tuna-concentrate efforts zetu kwenye maeneo hayo matatu tayari tupo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna eneo moja ambalo tunalisahau sana; tunalisahau lakini lina manufaa makubwa sana katika uchumi wa Taifa letu. leo walaji wakubwa wa nyama wako Middle East, wapo Mashariki ya Kati, na sisi tupo katikati ya Mashariki ya Kati na nchi ya Brazil. Ni kichekesho sana kuliona Taifa letu katika mwaka 2022 limesafirisha nyama tani elfu 10 pekee ilhali Brazil wamesafirisha tani za nyama milioni 2.9, ilhali tupo karibu zaidi na soko kuliko Brazil. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Mipango, kwenye vipaumbele na mwenyewe umetwambia kupanga ni kuchagua. Hatuwezi kufanya kila kitu, hatuwezi kuwa junk of all trades, lazima tuchague, umechagua utalii, umechagua misitu, umechagua madini, ninaomba uongeze nyama kwenye sekta hiyo. Na sababu, zipo wazi, kwanza, critical mass ambayo itapata faida kutokana na biashara hiyo; tunao wafugaji wengi tunachohitaji ku-coordinate ufugaji tupate nyama tukatumie hilo soko. Kwa hiyo, sehemu hiyo naomba iwe mchango wangu; kwamba, kwenye kupunguza nakisi ya urari wa biashara kwa kuongeza mauzo ya nje tuongeze na biashara hiyo, tuwe na vitu walau vinne, vinne vitoshe, kwa sababu tumevifanyia study kwamba vinaweza kuchangia uchumi mkubwa wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sehemu ya pili. Mheshimiwa Waziri hajasema, naomba nimuongezee kwenye mkakati wa kupunguza hiyo nakisi. Ameongelea zaidi kwenye kuongeza mauzo ya nje. Na nimesema kwenye hoja ya Kamati, imeeleza vizuri sana, changamoto ni mauzo yetu ya nje madogo, lakini pia tunaagiza bidhaa nyingi sana toka nje ya nchi unnecessarily. Tunalazimika tutoe dola yetu ya ndani tuipeleke nje tukanunue vitu ambavyo tuna uwezonavyo, tuna uwezo wa kuzalisha mafuta ya kula Watanzania, leo tuna…

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mhagama kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

TAARIFA

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa kaka yangu anayechangia hoja very scientific, Mheshimiwa Dkt. Mhagama, kwamba, nakisi iliyotajwa katika ripoti hii kwa Mkoa wa Singida peke yake kwa juhudi zilizofanywa na Serikali ya Rais huyu huyu chini ya Wizara ya Kilimo inayoongozwa na Mheshimiwa Bashe, uzalishaji wa mafuta, mbegu za mafuta na ukamuaji wa mafuta umepanda kwa kiwango ambacho kimesababisha sasa hivi bei ya mafuta imeshuka sana. Kwa hiyo, ninampa taarifa msemaji kwamba, moja ya bidhaa zilizotajwa zinazotoa fedha nyingi za kigeni ni uagizaji wa mafuta, na nchi mwaka huu imejitosheleza sana na uzalishaji wa mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa msemaji kwamba, achukue na hilo kuiambia Serikali hii sikivu kwamba habari ya kuagiza mafuta tunaweza tuka-adjust policy zetu katikati kulingana na uzalishaji mkubwa uliofanikiwa kutokana na juhudi kubwa za Wizara ya Kilimo. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa. Mheshimiwa Dkt. Mhagama, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. DKT. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nipokee kwa mikono miwili taarifa ya comred Kingu, mwamba na main campaigner wa ushindi wa Mheshimiwa Spika. Ninampongeza na ninamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ndio hoja yangu. Kwa sababu ya muda nimuombe Mheshimiwa Waziri, kwenye hoja namba sita, kwenye ukurasa ule wa 20 ameweka hoja namba sita ambayo inahusu kuongeza mauzo ya nje. Naomba aongeze hoja namba saba, kupunguza ununuaji wa bidhaa ambazo tunaweza kuzizalisha ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nina takwimu, lakini kwa sababu ya muda naomba nizitaje tu; mbolea mpaka mwaka jana, Mheshimiwa Bashe nampongeza sana, asilimia 12 ya mbolea tuliyotumia nchini tumezalisha ndani ya nchi hii. Asilimia inayobaki kama tani 617,000 bado zinaagizwa nje. Mheshimiwa Bashe umeshaweza kwa asilimia 15, unaweza kwa asilimia 80, we can make it. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili, petroli. Wizara ya Nishati mmepambana sana mna masuala ya gesi, n.k. Tupunguze uagizaji wa petroli, tutumie bidhaa zetu za ndani zinazoweza ku-solve, hizo ni alternative products. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye mafuta ya kula inatudhalilisha Watanzania kuona kwamba mpaka leo asilimia 60 ya mafuta tunayokula nchini tunaagiza kutoka nje, what a shame? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kwa Tanzania hatustahili hilo. Mheshimiwa Bashe umepambana kwenye eneo hilo. Mheshimiwa Waziri wa Mipango na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ongezeni nguvu kwenye sekta hiyo tuimalize na tuweze kutatua tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna eneo la ngano limefafanuliwa vizuri. Hayo ni mazo ambayo unapozidi kuyaagiza nje unawanyima Watanzania fursa ya masoko, unawanyima Watanzania fursa ya kukua, halafu unaendelea kuendeleza uchumi wan je wakati tuna nakisi kubwa ya fedha za kigeni kwa hiyo, tuna eneo la sukari na mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, sehemu ya mchango wangu nitaiandika na nitaiwasilisha Serikalini. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nikushukuru wewe binafsi kwa kunifanya kuwa mchangiaji wa pili kwa hotuba hii iliyotukuka ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii ambayo imebeba maudhui ya Wizara zote, imesheheni mipango na mikakati madhubuti ambayo kama itatekelezwa hivi ambavyo imewekwa, kwa hakika itatutoa Watanzania hapa tulipo leo na kutufikisha kwenye maisha ya uchumi wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Wazari Mkuu kwa hotuba hii nzuri, pia niwapongeze sana Wenyeviti wa Kamati zote mbili, ambao pia wameleta hotuba yao mbele ya Bunge lako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika tu kwamba kwa bahati mbaya nilitarajia nipate mawazo mbadala, lakini yameshindikana, hata hivi nadhani tutakwenda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikubaliane na mipango pamoja na mikakati yote ambayo hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imebeba. Maeneo ambayo nilipeda nitoe ushauri na niiombe Ofisi ya Waziri Mkuu kuifanyia kazi, katika kipindi hiki cha mwaka 2016/2017, moja ni Kitengo cha Maafa.
Katika hiki Kitengo cha Maafa kwanza nimpongeze sana Mkurugenzi wa Kitengo hiki kwa kazi yake nzuri anayoifanya mpaka sasa, licha ya changamoto alizonazo zinazoendana na ukosefu wa nyenzo za kufanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupitia makabrasha ya kitengo hiki, nilibaini kwamba pamoja na nia nzuri ya kitengo hiki kukabiliana na maafa, pamoja na jitihada nyingi zilizofanyika kuwajengea uwezo wanaofanya kazi katika kitengo hiki, bado kitengo hiki hakijawa na nguvu ya kutosha kuweza kukabiliana na changamoto za maafa katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe jitihada za makusudi zifanyike kuhakikisha kwamba kitengo hiki, pamoja na kujengewa uwezo wa kinadharia ambao kwa sasa wameendelea kujengewe kupitia miradi mbalimbali ingefaa pia kitengo hiki sasa kiwe na vituo maalumu vyenye nyenzo maalumu za kuweza kukabiliana na maafa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi ni kwamba wakati Dodoma na Kondoa wanalia kwelea kwelea responsiveness ya kitengo kinachohusu maafa ilikuwa ndogo sana, huu ni ushahidi kwamba bado tuna changamoto kubwa kwenye eneo hili, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu atusaidie kuhakikisha kwamba tunafanyia kazi ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nilipenda nichangie ni eneo la elimu. Wakati nachangia jana nilimueleza Mheshimiwa Spika kuhusu hali ya Jimbo langu la Madaba. Jimbo letu la Madaba ni Jimbo changa lina takribani miezi michache sana na Halmashauri ya Wilaya nayo ina miezi michache tu. Lakini upande wa elimu kama ilivyo katika maeneo mengine tuna changamoto nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao walimu zaidi ya 412 ndani ya Wilaya ya Songea, walimu hao Wilaya ya Songea inahusisha pia Halmashauri ya Wilaya ya Madaba, walimu hawajapandishwa madaraja kwa muda mrefu pamoja na kwamba wana hizo sifa. Nimeomba Chama cha Walimu kiniwasilishie nyaraka mbalimbali ambazo nitaziwakilisha katika Ofisi ya Waziri Mkuu ili mtusaidie kutanzua tatizo hili kwa sababu ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya elimu katika Halmashauri yetu na Wilaya ya Songea kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo ningependa nitoe mchango wa kina ni eneo la soko la mazao ya mahindi. Kama unavyojua Mkoa wa Ruvuma ni ghala la Taifa la chakula. Mkoa huu kwa miaka mingi umeendelea kuzalisha chakula cha kuwalisha Watanzania, katika Mkoa huu Halmashauri Wilaya ya Madaba, Jimbo la Madaba lina wakulima ambao wanazalisha sana mahindi ambayo yanachangia sana kwenye chakula cha Taifa letu. Kwa bahati mbaya mfumo wa manunuzi wa haya mahindi bado siyo rafiki kwa wananchi wale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa bado tunategemea kituo kimoja cha Madaba, yapo maghala katika kila Kata yanajengwa kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo na Chakula kwa kupitia mradi wa BRN. Maghala haya mpaka sasa hayajakamilika, na ujenzi wake umesimama kwa muda mrefuwakandarasi bado wanalalamika hawajalipwa.
Naiomba Ofisi ya Waziri Mkuu, wakati tunaendelea na mchakato huu tuhakikishe kwamba ule mchakato ambao umesimama katika vijiji vyote vya Halmashauri ya Wilaya Madaba ya kujenga na kuimarisha maghala ukamilike kwa sababu wananchi wa Jimbo la Madaba wataanza kuvuna mwezi ujao na watahitaji kuhifadhi mazao yao. kama ambavyo ulisema mwenyewe Mheshimiwa Waziri Mkuu ulipotembelea Mkoa wa Ruvuma, ulishauri kwamba NFRA wanunue mahindi katika vituo vilivyoko vijijini ili kuwaondolea Wananchi adha ya kusafirisha mazao haya kuyapeleka katika vituo maalum vya mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri yetu ya Madaba pia inachangamoto kubwa sana ya maji. Mji wa Madaba pekee na Kijiji cha Mkongotema ndiyo wenye maji yanayotiririka, lakini wingi wa mabomba hauwiani na idadi ya wananchi waliopo. Ipo miradi iliyofadhiliwa na World Bank, miradi hii imetekelezwa katika vijiji vitatu vya Mkongotema, Lilondo na Maweso. Kwa bahati mbaya miradi ya Maweso na Lilondo imesimama kwa muda mrefu sana, kwa vyovyote vile jitihada zilizofanyika mpaka sasa kubwa na niishukuru sana Wizara husika kwa kutufikisha pale ambapo tumefika. Ninaomba sana tunapoendelea na mchakato huu zoezi hilo pia la kukamilisha hii miradi ya maji katika maeneo yaliyobaki liendelee, lakini pia niombe sana Mji wa Madaba una kilio sana cha maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu, pamoja na Waziri wa Nishati na Madini, Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo ambao wamekuja ndani ya Jimbo langu na kushirikiana na wananchi kutatua kero zinazowakabili kwenye eneo la afya na eneo la umeme. Hivi ninavyokuambia Mheshimiwa Sospeter Muhongo yupo kwenye mchakato wa kukamilisha umeme wa maeneo ya Mji wa Madaba na Mungu bariki Disemba tutakuwa na umeme, ninaniomba sana zoezi hili liendelee, wananchi wa Madaba wanatambua sana juhudi za Mheshimiwa Sospeter Muhongo, lakini pia wanatambua sana jitihada za Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu za kuhakikisha kwamba Madaba tunapata Hospitali ya Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho na la muhimu sana ni kwamba tulipokuwa tunaelekea uchaguzi wa mwaka 2015 vipo vijiji vingi vilivyozaliwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Madaba kama ambavyo vilizaliwa katika maeneo mengine ya Songea Vijijini. Vijiji hivi bado havijapata usajili wa kuduma na kama vimepata havija…
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napongeza sana hotuba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba Madelu. Hotuba hii imesheheni mipango na mikakati madhubuti ya kuliondoa kundi la Watanzania wafikiao asilimia 80 na kuwafikisha kwenye uchumi wa kati. Umadhubuti wa Mipango na Mikakati iliyopo katika hotuba hii ni kielelezo cha umadhubuti wa Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba. Napenda nimthibitishie kuwa wananchi ninaowawakilisha, Jimbo la Maduba wanatambua sana umahiri na umadhubuti wa Mheshimiwa Mwigulu Nchemba.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nielekeze mchango wangu katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ni matumizi ya mbegu bora za kilimo. Kadiri ya Utafiti wa Masalwala (2013), asilimia 93 ya mbegu zinazotumiwa na wakulima katika misimu mbalimbali ni recycled from previous crops. Hii inatokana na gharama za mbegu hizo, upatikanaji, ubora wa mbegu hizo na uelewa wa wakulima juu ya matumizi na umuhimu wa mbegu hizo. Napongeza kuwa Wizara imeliona hilo na tayari imejipanga kuongeza uzalishaji wa mbegu kutoka tani 10,270.86 hadi tani 40,000 ikiwa ni mara nne. Ni hatua kubwa sana. Naomba Wizara isimamie hili, tujipime kwa kiasi hiki na mwaka ujao twende mbali zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ni muhimu katika mikakati ya kufanikisha zoezi hili, makampuni ya ndani yapate kipaumbele kujengewa uwezo wa kuzalisha mbegu. Yapo makampuni yenye nia na yamethubutu kuanza. Ni vema yakapata ruzuku kuyawezesha kuzalisha mbegu za mazao ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili ni mfumo wa upatikanaji wa pembejeo. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba kwa kuamua sasa kupitia upya mfumo wa usambazaji wa pembejeo kwa kuzingatia malalamiko makubwa ya mfumo wa sasa wa ruzuku. Mkakati huu mpya ni mzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yangu ni kuharakisha mapitio haya. Case studies ni nyingi, zipo Asasi na wadau wengi waliojaribisha models mbalimbali. Miongoni mwa wadau hao ni AGRA, SNV, RUCODIA, RUDI, BRTENS na kadhalika. Wadau hawa tayari wana models mbalimbali za usambazaji wa pembejeo. Jambo muhimu ni kwamba mfumo mzima wa usambazaji pembejeo uwe enterprise led. Ni vema Wizara ikakutana na wadau hao na kuchukua uzoefu wao katika suala zima la Agro-Dealers Development.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu ni mazingira wezeshi ya kilimo-biashara. Hotuba ya Mheshimiwa Mwigulu imefafanua vizuri mazingira wezeshi ya kilimo-biashara. Katika aliyosema Mheshimiwa Waziri, ningependa kuongeza yafuatayo:-
(i) Mafanikio ya kilimo yanategemea sana mafanikio ya miundombinu ya barabara vijijini, upatikanaji wa rasilimali fedha na elimu ya kilimo; na
(ii) Model ya mradi wa MIVARF uliopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni nzuri sana ya comprehensive approach ambayo kama Wizara itachukua model hizi, maendeleo ya kilimo chenye tija tutayapata kwa haraka sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nne, Chuo cha Mafunzo ya Mifugo LITA (Madaba). Tunaomba chuo hiki kitoe pia mafunzo ya kilimo na kipandishwe hadhi na kuwa chuo kikuu kwani Mikoa ya Kusini mahitaji yetu katika eneo hilo ni makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. KIZITO M. JOSEPH: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia muda niliopewa niende moja kwa moja, kwanza kutoa salamu za shukurani kwa Waziri, Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo, ambaye majira ya jioni kuelekea saa moja, mvua zinanyesha, amechoka, amefanya kazi kutwa nzima Ludewa, anarudi anakwenda Songea Mjini, alikubali kuendesha mkutano Madaba. Wananchi wa Jimbo la Madaba hawataisahau ile taswira.
Mheshimiwa Naibu Spika, siku ile Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo, alitoa majibu ya moja kwa moja ya tatizo kubwa la umeme la wananchi wa Madaba. Wananchi wa Madaba wanamshukuru na wapo pamoja naye katika safari hii ya kutekeleza majukumu aliyopewa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto katika utekelezaji wa maagizo ya Mheshimiwa Waziri, lakini changamoto hizi zinahusisha zaidi muundo wa utaratibu huo wa utekelezaji. Kwa utaratibu ambao Mheshimiwa Muhongo ameuweka, ni kwamba Madaba ifikapo Desemba tutapata umeme, lakini katika kipindi hiki cha miaka miwili Madaba Mjini patakuwa hub ya umeme unaotoka Makambako kuelekea Songea, lakini pia hub ya umeme unaotoka Mchuchuma na Liganga kulelekea maeneo mengine ya Taifa letu. Maana yake nini? Maana yake Madaba inakwenda kupitia transformation kubwa sana ya uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto inayotupata kwa sasa ni kwamba Serikali bado ina ugumu kidogo wa kuchangia gharama kuweza ku-meet gharama za wafadhili kwenye hilo jukumu na kikwazo kinaonekana kipo Hazina. Naomba watu wa Hazina wasikalie pesa kama zipo. Kama pesa zipo na zimepangwa kwa matumizi hayo, basi zitolewe zikafanye hizo kazi ili hizi Wizara husika ziweze kujibu matatizo ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita kwenye hili tu kwa sababu linanigusa na wananchi wa Madaba lina wagusa sana. Ndani ya Jimbo langu la Madaba ni kijiji kimoja tu cha Lilondo kina umeme na umeme huu ni wa wananchi. Nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Mwijage, ambao kwa namna moja au nyingine wamesaidia sana kupatikana ule umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote ya Jimbo la Madaba, Vituo vyote vya Afya, saa hizi mimi Mbunge kwa kutegemea posho ninazopata hapa Bungeni, naweka solar. Hata ukiiangalia gari ninayoitembelea ni ya kawaida sana ili niweze kubana matumizi ya kupata solar kwa ajili ya Vituo vyote vya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana na wananchi wa Jimbo la Madaba wanaomba sana kwa Mheshimiwa Waziri Profesa Sospeter Muhongo, kwamba yale ambayo ameyapanga wanamwomba Mwenyezi Mungu amjalie nguvu ili ifikapo Desemba na kuendelea changamoto hii iwe imekwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo miradi ya kielelezo ya kiuchumi. Ndugu yangu…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nakushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi. Pili, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa uwasilishi wake mzuri. Pamoja na kazi nzuri aliyoifanya Mheshimiwa Waziri nina mambo mawili, matatu ya kuishauri hii Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, unajua habari ya viwanda Tanzania siyo habari ngeni. Tumekuwa na viwanda miaka ya 80 kuelekea miaka ya 90 na viwanda vingi vimekufa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri, sehemu pekee au mkakati pekee ambao ameuweka ambao umeonekana wa namna ya kulinda viwanda vya ndani ni kuongeza kodi kwenye bidhaa zinazotoka nje, zile bidhaa ambazo tunaweza kuzizalisha ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maoni yangu huo ni mkakati mzuri, lakini mkakati huu pekee hautatosha kulinda viwanda vya mafuta ya kula, hautatosha kulinda viwanda vya sukari nchini, hautatosha kulinda viwanda vya nguo nchini. kwa sababu kikwazo cha viwanda vya Tanzania siyo tu ushindani wa bei za bidhaa zinazoingia, bali pia mikataba ambayo tunaingia na nchi marafiki ambao tunafanya nao biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vyovyote vile, mikataba ile bado inatubana. Pengine hata kuweka hizo kodi kwenye hizo bidhaa huenda tukagomewa na wadau marafiki tunaofanya nao biashara kwa sababu na wao wanataka kulinda viwanda vyao. Kwa hiyo, naishauri Wizara ya Fedha ifanye kazi ya kina. Mwezi wa Pili nilitoa ushauri huu na sasa narudia tena kwa sababu mpaka sasa sijaona assessment ya kutosha ya ku-assess kwa nini tulifeli miaka ya 1980 na 1990 na kwa nini tunadhani tutafaulu katika kipindi hiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ni suala zima la maji. Sera ya Taifa inatutaka Watanzania wote popote walipo waweze kupata maji katika umbali usiozidi mita 400. Ukiiangalia sera hii na mpango mkakati uliowekwa na Wizara ya Fedha, havifanani kabisa. Kukata sh. 50/= kwenye mafuta ya petrol na diesel pekee, havitoshi. Kamati ya Bajeti imeshauri tuweke angalau sh. 100/= na baadhi ya Wabunge wameshauri tuweke angalau sh. 100/=. Nami naomba tuweke angalau sh. 100/= ili tuweze kusogea mbele kwa haraka zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Madaba ni moja katika Majimbo ambayo yana tabu sana ya maji. Hivi ninavyoongea, Kijiji cha Lilondo na Maweso toka miradi imeanza mwaka 2015, haijakamilika na Wakandarasi bado wanahangaika kulipwa. Naishukuru Wizara ya Maji, tunawasiliana kwa jambo hili, lakini huu ni ushahidi kwamba kuna matatizo ya kutosha kwenye hili eneo, tulitengee bajeti ya kutosha kwa kuzingatia ushauri wa Kamati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni ombi kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango avae viatu vya Walimu wa Sekondari na Shule za Msingi ambao katika uhai wao wote wanalitumikia Taifa hili, mishahara yao inakatwa kodi na wanapomaliza kipindi cha utumishi wanalipwa kiinua mgongo na kinakatwa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri avae viatu vya watumishi wengine wa Serikali na Sekta ya Umma ambao mishahara yao ni ya chini, wanakatwa kodi, wanafanya kazi, lakini wanapomaliza utumishi wao, bado kiinua mgogo kinakatwa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge lililopita lilienda hatua mbele, likaiomba Serikali iondoe kodi kwenye hivi viinua mgongo, yaani kwenye mafao ya wafanyakazi. Nilitegemea Wizara ya Fedha ije na mkakati huo sasa wa kuondoa hizo kodi kwenye mafao ya wafanyakazi na kupendekeza njia mbadala ya kupata fedha kwa ajili ya kuendeshea Serikali, kwa sababu hawa wafanyakazi wameendelea kukatwa kodi wakati wote. Kilichonishangaza, tunazidi kurudi nyuma. Tulishapiga hatua mbili mbele, tunarudi hatua nne nyuma, tunaanza sasa kufikiria kukata kodi kwenye mafao ya Wabunge. Tunakwenda wapi? Tutafika lini tunakotaka kwenda kuwatengenezea Watanzania maisha bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri avae viatu vya Wabunge wanaotoka katika Majimbo yenye changamoto kama Jimbo la Madaba. Mbunge wa Madaba akishapata posho humu Bungeni, anakwenda kununua solar kuweka kwenye Vituo vya Afya. Anakwenda kuchangia maji Matetereka ili wananchi wapate maji kwa sababu Serikali bado haijaweza kufikia wananchi hao.…
Nasikitika sana ninapoambiwa kwamba...
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, kuhusu vikwazo vya kufikisha pembejeo (mbolea, viatilifu na mbegu bora) kwa wakulima wadogo vijijini na hivyo kupoteza tija; wakulima wengi wadogo wapo vijijini ambako ndiko pia shughuli za kilimo zinafanyika. Maduka ya pembejeo kwa sehemu kubwa yapo mijini. Tanzania mkulima mdogo apate pembejeo ni lazima asafiri hadi mjini kununua. Hili linaongeza gharama za uzalishaji kwa mkulima mdogo.

Mheshimiwa Spika, ili kuongeza tija haina budi maduka ya pembejeo yasambae hadi vijijini ambako wakulima wapo. Katika maeneo mengi wajasiriamali vijijini wanafanya jitihada za kufungua maduka ya pembejeo ili kufikisha huduma karibu na wakulima. Jitihada hizi zinakwamishwa na gharama kubwa za vyeti vinavyotakiwa. Vyeti ni kama ifuatavyo:-

(1) TOSCI = 100,000.
(2) TPRI = 320,000.
(3) TFRA = gharama ya chakula wakati wa mafunzo. (4) TFDA = 100,000.
(5) Leseni = 71,000.

Jumla ni 591,000

Mheshimiwa Spika, gharama hizi ni kubwa sana, zinakatisha tamaa kwa wajasiriamali. Wapo wengi wameshindwa licha ya kushiriki mafunzo na kujengewa hamasa bado wameshindwa kufungua maduka. Mifano halisi ni, katika Mkoa wa Kagera wajasiriamali 461 walijengewa hamasa na kupata mafunzo ya biashara hiyo kupitia Shirika la AGRA matokeo yake ni kama ifuatavyo:-

Waliopata mafunzo na kujengewa hamasa ni 461, Cheti TOSCI (82), Cheti TFRA (108), Cheti TPRI (17), WALIOFUNGUA MADUKA (139)

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Kigoma, kati ya Wajasiriamali 704 waliojengewa hamasa na kupatiwa mafunzo ya biashara na Shirika la AGRA ni wajasiriamali 389 tu ndiyo wamefungua maduka. Aidha, wajasiriamali 159 walipata mafunzo na TFRA Mwezi Oktoba, 2018 lakini hadi leo hawajapata vyeti vya TFRA ili kuwezesha kuanzisha maduka ya pembejeo vijijini. Utaratibu huu kama hautabadilika, ukuaji wa sekta hii utaendelea kudorora.

Mheshimiwa Spika, ushauri; Serikali iangalie upya ada hizo (TOSCI, TFRA, TPRI, TFDA) ziangaliwe upya au Serikali ibebe huo mzigo ili kuwezesha ufikishaji mbolea, viatilifu, mbegu bora kwa wakulima wadogo.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza kabisa nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mpango kwa kuleta mwelekeo wa Mpango huu, ili ujadiliwe na Bunge lako na mimi kupata nafasi ya kutoa mawazo yangu, lakini nasikitika itabidi nitumie sehemu ya muda wangu mzuri kuweza kueleza maeneo ambayo pengine yalikuwa very obvious.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya michango yetu inaonesha kwamba baadhi ya Wabunge tume-panic na Wabunge wengi tulio-panic tunaufanya umma wa Watanzania u-panic. Na ukifuatilia vitu vinavyotufanya tu-panic vinakosa mantiki na leo mbele ya Bunge lako Tukufu nalazimika kuongea kwa kutumia analogia kwa sababu ndio namna pekee ambayo nadhani nitaeleweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka kadhaa iliyopita hapa Dodoma watu wote wakiwemo Wabunge walikuwa wanakutana pale Chako ni Chako wanakula kuku. Miaka mitatu/minne baadaye sehemu mbalimbali zinazotoa huduma kama za Chako ni Chako zimefunguliwa na wateja wanachagua sehemu za kwenda, it is very natural. Miaka kadhaa iliyopita, labda kabla sijafika huko, kama unaishi mtaani, nasema ninatumia analogia, lugha rahisi kabisa na mifano rahisi, kama unakaa mtaani na katika mtaa wako unapakana na mitaa mingine minne/mitano katika mitaa hiyo mitano hakuna baa, kuna baa moja tu katika mtaa wako watu wote wanaokunywa katika maeneo hayo watakunywa katika baa yako, lakini siku mtaa wa tatu wamefungua baa tabia ya walevi ni kwenda kujaribu katika baa nyingine pia. Lakini wakiwa kule wataweza kulinganisha na ubora wa huduma ya baa yako; hiyo ndio lugha ya analogia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaendesha Bandari yetu ya Dar es Salaam bandari nyingine zimefuata baadae na kwa kawaida kwa tabia ya watu hupenda kujaribu. Leo bandari nyingine zipo kwa vyovyote vile huwezi kubaki na wateja wale wale ambao ulikuwanao kwa kipindi chote. Hiyo ni lugha rahisi, Watanzania tusiyumbishwe na kauli za baadhi ya Wabunge kuonyesha kwamba sababu za kupungua mizigo bandarini zinahusiana moja kwa moja na mambo ya kodi, si kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, hilo haliondoi jukumu la Waziri wa Fedha kuendelea kuchunguza sababu mbalimbali za kupungua wateja, lakini sababu nyingine ndio hizo. Lazima kazi ya ziada ifanyike ili kuweza kuvuta wateja zaidi na kuweza kuimarisha bandari yetu ili iweze kuchangia mapato zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana kuona baadhi ya Wabunge tunawalilia wafanyabiashara makanjanja. Ni ajabu kuona kwamba katika bandari ile ile ambayo tunasema kwamba mizigo imepungua, mapato yameongezeka, mantiki yake ni nini? Mantiki yake ni rahisi tu, wale ambao walizoea ubabaishaji wameenda kubahatisha maeneo mengine labda wakabahatishe kubabaisha. Lakini wafanyabiashara makini wanaendela kutumia bandari yetu na hao ndio wanaotupa mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la msingi kwenye eneo hilo ni upotoshwaji wa mantiki nzima ya kusimamia matumizi na kukusanya kodi. Humu ndani baadhi yetu wametafsiri kama kubana matumizi; sijaona mantiki, bajeti ya mwaka jana tunayoimaliza mwaka huu ni shilingi trilioni 29 na mpango huu unatupeleka kwenye shilingi trilioni 32. Hiyo sio kubana matumizi, Serikali ya Awamu ya Tano inachokifanya ni kusimamia matumizi, kuna utofauti kati ya kubana matumizi na kusimamia matumizi. Serikali inachokifanya ni kuhakikisha inaongeza efficiency katika matumizi ya fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale maeneo ambayo hayana tija Serikali imepunguza kupeleka pesa na badala yake imepeleka maeneo yenye tija zaidi. Kwa hiyo, Watanzania tuelewe kwamba hatujabana matumizi isipokuwa tunapeleka fedha maeneo yenye tija zaidi, maeneo ambayo yatakuza uchumi zaidi na ndio maana bajeti imetoka toka shilingi trilioni 29 kwenda shilingi trilioni 32, hiyo ndio mantiki, ni kusimamia matumizi. Sasa wale waliozoea fedha rahisi, wale waliozoea ubabaishaji hilo nalo linawaumiza. Niwaombe Watanzania makini, wanaolipenda Taifa hili wamuunge mkono Mheshimiwa Rais katika jambo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuhakikishia katikati ya giza nene ndipo inakaribia asubuhi, hapa tulipo ndipo wakati sahihi kunakaribia kucha. Mheshimiwa Zitto Kabwe alisema lazima kuwe na maumivu tunapotaka kufanya mabadiliko makubwa kama haya. Tukumbuke miongoni mwetu baadhi ya Watanzania walizoea fedha rahisi, walizoweza leo anaanzisha biashara ya shilingi milioni 10 na kila mwezi anapata faida ya shilingi milioni tano kwa sababu, alikuwa anakwepa kodi. Tumueleze mantiki ya kodi na tumueleze kwamba biashara zinakuwa steadly, hatua kwa hatua. Watanzania makini hawana tatizo na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Mpango atoe ushirikiano na Mawaziri wengine waendelee kuasimamia matumizi ya Serikali na kuelekeza pesa katika maeneo yenye tija zaidi kwa Watanzania. Hilo lilikuwa kuweka tu mazingira sawa kwa sababu niliona linapotoshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa ambalo leo nilitaka nichangie ni dhana nzima ya kukuza viwanda. Katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi tumeweka bayana aina gani ya viwanda vitatutoa Tanzania kwa haraka zaidi. Tulisema tuwekeze kwenye viwanda vinavyosindika zaidi mazao ya kilimo kwa lengo kwanza la kumuwezesha mkulima mdogo apate soko la mazao yake, lakini pia kutoa ajira kubwa zaidi kwa Watanzania. Katika mpango tulioupata hilo halijawekwa bayana, tumeongelea viwanda vya General Tyre, tumeongelea viwanda vingine ambavyo kimsingi havigusi asilimia 80 ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosikitika kwenye mpango huu ni kwamba hatujaoanisha vizuri ile Ilani ya Chama cha Mapinduzi na huu mpango. Tunapowekeza nguvu nyingi kwenye kushughulikia viwanda tumesema ni jambo zuri, Magadi ya Soda - Bonde la Engaruka, tumeongea viwanda chini ya TEMCO na nini, lakini viwanda hivi katika ujumla wake haviendi kutatua tatizo la ajira kwa vijana wetu walio asilimia kubwa na wala haliendi kutatua tatizo la soko la mazao yetu ya kilimo. Kwa hiyo, niishauri sana Serikali kwenye hili lazima turudi tukafanye kazi upya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine kwa haraka haraka, tunahangaika sana na soko la mahindi ni vema katika mpango huu sasa ikawekwa bayana. Kinachomfanya mkulima akalime ni bei ya mazao. Tunatoa ruzuku, lakini bado wakulima hawazalishi kwa tija kwa sababu hawapati faida katika uzalishaji wao. Ipo haja sasa ya kuja na sera madhubuti itakayomfanya mkulima mdogo wa Tanzania awe huru kuuza mazao yake kokote na wakati wowote. Leo ukienda kila mahali pikipiki zimejaa, Serikali imetoa ruzuku sana kwenye power tiller, lakini huzioni kokote kwa sababu hazina manufaa
kwenye kilimo chao, lakini watu wangapi wananunua yebo yebo kwa sababu hizo bodaboda kwa sababu wanajua zinawalipa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutajenga mazingira mazuri kwenye sekta ya kilimo hatutahitaji kugharamia mbolea za ruzuku tena. Tujenge mazingira yenye ushindani kwenye sekta ya kilimo, tuwaache wakulima wadogo wauze mazao yao wanakotaka, anayetaka kupeleka Malawi, anayetaka kwenda Zambia na kama Serikali inataka kununua iingie kwenye ushindani. Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumemuwezesha sana mkulima mdogo na wala hatutahangaika habari za kutafuta pembejeo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia muda ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru wewe lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2017/2018. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mmoja kati ya Wabunge waliobahatika kuwa katika Kamati ya Katiba na Sheria, Kamati ambayo inafanya kazi kwa karibu sana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara zote zilizopo chini yake. Tumebahatika kujua mambo mengi na kujifunza mengi na nikuthibitishie kabisa kwamba Ofisi hii na Wizara zake zote wapo vizuri sana katika kuwatumikia Watanzania. Nikuombe wewe na Bunge zima kuunga mkono jitihada za Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa kuzingatia muda naomba nijikite kwenye eneo moja muhimu sana ambalo linagusa asilimia 90 ya Watanzania ambalo liko katika ukurasa wa 21 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu kulimo. Kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya 2012 asilimia 85 - 90 ya Watanzania tunaishi kwa kutegemea kilimo au moja kwa moja, kibiashara au kwa namna nyingine lakini asilimia 90 ya Watanzania tunategemea kilimo. Kwa mujibu wa sensa ya kilimo na mifugo ya hivi karibuni inatupa takwimu hizo za asilimia 85 - 90 lakini sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 inatueleza idadi ya Watanzania ambao tupo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 21 kwa taarifa tulizonazo, uzalishaji wa mazao ya chakula kwa msimu wa mwaka 2015/2016 ukijumuisha mazao ya nafaka na yasiyo ya nafaka tumezalisha jumla ya tani milioni 16. Tani hizi milioni 16 maana yake zimezalishwa na asilimia 85 ya Watanzania kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012. Kama hivyo ndivyo maana yake kila Mtanzania anayetegemea kilimo amezalisha tani 0.34 au sawa na gunia nne tu za mahindi kwa mwaka mzima wa 2015/2016. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaambiwa ziada ya mazao ya nafaka na yasiyo ya nafaka ni tani milioni tatu. Tukizigawa kwa idadi ya Watanzania wanaotegemea kilimo ambao ni asilimia 85 tunapata ziada ya tani 0.07 ambayo sawa na gunia moja tu la ziada. Kwa hiyo, ukiangalia kwa takwimu hizi maana yake Watanzania tunaotegemea kilimo asilimia 85 - 90 kila kaya au kila mtu amezalisha gunia nne za
mahindi na ametumia gunia tatu kwa chakula na amebaki na ziada ya gunia moja. Tanzania ya viwanda hatutaweza kuifikia kwa kasi hiyo ndogo kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa kwa nini asilimia kubwa ya Watanzania hatuna pesa mifukoni ni kwa sababu ziada yetu ni ndogo sana tani 0.07 kwa maana ya gunia moja tu la mahindi kwa mwaka mzima sawa na Sh.35,000 – Sh.50,000. Ziada hii ni ndogo maana yake kilimo katika Taifa letu kinakua taratibu mno.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tumefika hapo? Kwa nini uzalishaji wetu uwe mdogo kiasi hicho? Tani milioni 16 za chakula siyo jambo la kujivunia. Tumefika hapo kwa sababu kubwa mbili. Moja, kilimo chetu hakina dira. Watanzania na taifa hatujui kwenye sekta ya kilimo tunatafuta nini. Tuna maneno ya jumla ya kusema kwamba tunataka ku-address food security, very good. Kwenye food security tumefaulu, Tanzania hakuna njaa mgawanyo wa chakula ukiwa vizuri kila kaya ina uwezo wa kujilisha, kwa hiyo, kwenye hilo tumefaulu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini malengo yetu kwenye sekta ya kilimo siyo ku-address food security pekee. Sekta ya kilimo pamoja na kuwa inakwenda ku-address food security kwa maana ya uhakika wa chakula, sekta hii ya kilimo inawaajiri Watanzania asilimia 90. Kwa hiyo, lazima tutoke hapo kwenye food security twende sasa kukifanya kilimo chetu kiwe biashara na kiwe chanzo cha mapato kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Serikali tumefanya vizuri kwenye suala zima la uhakika wa chakula lakini bado tuna kazi sasa ya kuwafanya asilimia 85 - 90 ya Watanzania wanaotegemea kilimo waweze kujiajiri katika sekta hiyo. Kwa hiyo, ni vizuri sasa Wizara ya Kilimo itoe dira ni nini kama Taifa tunataka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ni kwamba kilimo chetu siyo demand driven, hatulimi kwa kuzingatia mahitaji ya soko. Kama tunataka kujitosheleza kwa chakula tulime mazao gani na kwa kiwango gani, uwezo wetu wa ndani wa ku-consume kile ambacho tunazalisha ni upi na
ziada tunaipeleka wapi. Tumeona sekta ya kilimo inayumba sana kwenye eneo la masoko. Mara tunafunga mipaka tusipeleke mazao nje, mara tunafungua mipaka, hatuna uwezo wa ku-forecast production zetu katika sekta hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo ni tatizo na napenda sana Wizara inayohusika ichukue muda wa kutosha kufanya consultation na wataalam mbalimbali lakini hasa na Wabunge wa Bunge hili kwa sababu Wabunge hawa ndiyo wanaoishi na wananchi, ndiyo wanaojua matatizo ya wananchi na sisi ndiyo tunaolima mahindi, maharage, mpunga, soya na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la pili kwenye sekta ya kilimo ni uwezeshaji katika sekta hii umekuwa mdogo sana na uwezeshaji huu wakati mwingine umekuwa holela usiozingatia mahitaji halisi. Serikali imebeba mzigo mkubwa sana wa kuhakikisha kwamba Watanzania tunapata pembejeo zenye ubora ikiwemo mbolea na kadhalika na zinakwenda kusaidia kuzalisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kukushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi na nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu sana ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia katika maeneo makubwa mawili na iwapo muda utaniruhusu, nitaongeza sehemu ya tatu. Kwanza kabisa, niungane na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamempongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya kwa kupitia Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Nisingependa kurudia maneno mazuri ambayo Wabunge wengi wamesema kuhusu kazi nzuri zilizofanyika, Tanzania sasa imeunganishwa kwa barabara nyingi, inaunganishwa kwa reli, lakini inaunganishwa kwa anga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kutambua mchango mkubwa sana wa Mawaziri kwa kumsaidia Mheshimiwa Rais na kesho sisi wadau wa Mkoa wa Ruvuma tutakuwa pale Songea tarehe 30 kupokea ndege aina ya Bombardier ikitua kwa mara ya kwanza katika Mji wa Songea. Kwa hiyo, ni kazi nzuri ya Wizara hii, nachukua nafasi hii kuipongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo matatu ambayo napenda niishauri Wizara au Serikali katika ujumla wake. Eneo la kwanza, hii miradi tunayowekeza ni mikubwa sana. Wizara ya Nishati inawekeza katika miradi mikubwa sana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano nao wanawekeza katika miradi mikubwa sana. Wizara hizi mbili, ili miradi hii inayowekezwa iweze kuwa na tija, ni muhimu sana hizi Wizara mbili zikafanya kazi kwa ukaribu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua sisi Jimbo la Madaba tunapakana na eneo lenye mradi mkubwa sana, tunaita Flagship Projects pale Liganga na Mchuchuma. Huu ni mradi mkubwa sana na ni mradi ambao umezungumziwa kwanza kabisa na Mheshimiwa Profesa Simon Mbilinyi, baadaye akafuatia Mheshimiwa Waziri Jenister Mhagama. Mimi leo ni Mbunge wa tatu katika Bunge lako kuzungumzia mradi huu kutoka eneo hilo hilo la Jimbo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu umechukua muda mrefu sana, lakini sasa mradi huu una matumaini makubwa ya kuanza; na taratibu zote za kuanza zimekamilika na tutaisikia kwenye Wizara wa Nishati na Madini watakapowakilisha. Kinachosikitisha ni kwamba hakuna maandalizi ya kutosha kuhakikisha kwamba barabara zinazokwenda kwenye mradi huu mkubwa zinakamilika. Huwezi kuzungumzia Mradi wa Lingaganga na Mchuchuma bila kuzungumzia barabara inayotoka Madaba kwenda Mkiyu - Linganga. Utawezaje kusafirisha mitambo kwenda katika eneo la mradi? Utawezaje kuvuna makaa na chuma kutoka katika eneo la mradi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, yawezekana Wizara kwa sababu moja au nyingine na yawezekana ni sababu za msingi kwamba hawajaweka bajeti ya kutosha ya kukamilisha barabara hii kwa kiwango cha lami, nawaomba Wizara, kama kweli tupo serious na kama kweli Miradi ya Mchuchuma na Linganga inaanza, lazima barabara ya Madaba - Mkiyu ikamilike. La sivyo, tutaiingiza Serikali kwenye hasara kubwa sana. Mradi upo tayari kuanza lakini barabara ya kwenda kwenye mradi haipo. Hatuwezi kufanikiwa tusipoweza kuunganisha haya mambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili linahusu Mfuko wa Barabara Vijijini. TAMISEMI wanapata asilimia 30 ya fedha zote zinazokusanywa kwa ajili ya Mfuko wa Barabara na asilimia 60 inabaki kwa TANROADs kwa ajili ya kushughulikia barabara za mikoa na hii asilimia 30 inakwenda TAMISEMI na inakuwa translated kwenye kutekeleza miradi ya barabara ndani ya Halmashauri. TAMISEMI wanakuja na wazo kwamba tuwe na Rural Road Agency, hili wazo ukiliangalia kwa haraka, linaonekana kama ni zuri na lenye tija, lakini niliomba ni-draw attention ya TAMISEMI na Wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano. Kwanza lazima tujue kwamba kama kumekuwa na ufanisi katika ngazi za Halmashauri zetu, ni kwa sababu wale wanaofanya kazi katika Halmashauri za Wilaya wapo accountable moja kwa moja kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hiyo sense of accountability ndiyo inayofanya Halmashauri zetu ziwe na tija (efficiency) kwa sababu anayesimamia miradi katika Halmashauri ni Diwani ambaye yupo karibu na wananchi, anajua matatizo ya wananchi na anawajibika kwa wananchi. So sense of accountability imeleta tija sana katika utekelezaji wa miradi katika ngazi ya Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukilinganisha na taasisi au agency mbalimbali zinazoundwa zenye hadhi ya Kitaifa sense of accountability haiwezi kuwa sawa. Halmashauri sense ya accountability ni kubwa zaidi. Naomba sana, tusi-attempt kutengeza huu Mfuko wa Barabara Vijijini, isipokuwa fedha hizi zigawanywe kwa uwiano sawa katika Halmashauri na ziendelee kusimamiwa na Halmashauri za Wilaya zetu. Italeta tija zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine najua TANROADs hakuna urasimu sana, lakini taasisi yoyote yenye muundo ina urasimu. Halmashauri zina urasimu, TANROADs wana urasimu na Taasisi yoyote ina urasimu kwa sababu ya muundo wake. Sasa ukilinganisha level ya urasimu katika Taasisi za Kitaifa na Halmashauri, Halmashauri level ya urasimu ipo chini sana. Kwa hiyo, tutumie hiyo fursa sasa kupeleka hizi fedha zikafanye kazi kwa tija katika Halmashauri, tukiziacha kwenye ngazi hizo za juu hatutapata ufanisi. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, pia ningeweza kusema, kwangu mimi kufikiria kutengeneza hii tunayoita Mfuko wa Barabara Vijijini kwa maana ya Rural Road Agency, katika context ile ile na mfananisho ule ule wa TANROADs ni jaribio la kudhoofisha dhana ya ugatuzi wa madaraka. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ifanye study upya ya efficiency za Halmashauri zetu ukilinganisha na efficiency ya agency mbalimbali zenye hadhi ya Kitaifa ili kuleta tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kama muda unaniruhusu, nichangie tu kwamba ukisoma katika hiki kitabu unaona kumekuwa na shida kidogo katika allocations za projects. Ipo mikoa ambayo imepata miradi mingi zaidi kuliko mingine. Sababu zinaweza zikawa za msingi kwa maana ya mahitaji halisi, lakini ni vizuri sasa niiombe Serikali iangalie priorities nyingine pia.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tumewekeza fedha nyingi sana kujenga Jiji la Dar es Salaam ambalo lina wananchi milioni tatu na zaidi kidogo…
Wanakaribia milioni tano, lakini tukumbuke pia mahitaji katika maeneo mengine ni muhimu pia. Naiomba Serikali sasa iangalie, ifanye rationalization ya miradi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile muda hauniruhusu, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wote, wanaompongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri sana anayoifanya kwa Watanzania.

Pili, nipongeze sana Serikali kwa kuleta mpango huu na bajeti hii ya mwaka 2017/2018. Ni bajeti ya kipekee sana ambayo inagusa maeneo yote makubwa ambayo kama ya tatekelezwa vizuri, yatawatoa Watanzania na kuwafikisha kwenye uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maslahi ya muda, kwanza niishukuru sana Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kuitazama kwa namna ya pekee sana Halmashauri yetu ya Wilaya ya Madaba na Jimbo la Madaba. Kimsingi kushukuru ni kuomba tena, wana Madaba katika kipindi hiki cha mwaka mmoja, tumeona maendeleo makubwa sana katika maeneo mbalimbali ikiwemo afya, maji, nishati na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri na Wizara zenu, lakini zaidi Mheshimiwa Rais ambaye amewakabidhi haya majukumu. Wana Madaba tunatambua mchango mkubwa wa Serikali kwa maendeleo yetu na ninaamini tutaendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali hii kwa sababu tunaamini ndani ya kipindi cha miaka mitano wana Madaba tutakuwa tumepiga hatua kubwa sana ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango mkubwa ambao nilitaka niutoe kwako na kwa Wabunge leo hasa kwa Serikali, ni mahusiano ya kilimo na Tanzania ya viwanda. Kwa Muktadha wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2015/2020. Ukitazama katika Ilani yetu, kipaumbele cha Awamu ya Tano ni kuwa na viwanda Tanzania nzima ili kutoa ajira kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sehemu kubwa Serikali imeweka misingi imara ya kutengeneza au yakujenga Tanzania ya viwanda. Miaka miwili tu baada ya kuanza Serikali hii au mwaka mmoja na nusu, tayari tunaona viwanda vingi vinajengwa. Hata hivyo ninaomba niikumbushe Wizara na niikumbushe Serikali kwamba aina ya viwanda vinavyojengwa, pamoja na kwamba ni viwanda vizuri, lakini aina hii bado haiendi kujibu kwa namna inavyotakiwa mahitaji makubwa ya Watanzania wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi, inatutaka aina ya viwanda ambavyo vinatakiwa tuvijenge sana ni vile ambavyo vitaongeza thamani ya mazao yetu na hivi kutoa soko na kuongeza kipato kwa mwananchi mkulima.

Tukumbuke kwamba Watanzania asilimia 80 tunaishi kwa kutegemea kilimo, tunategemea masoko mazuri ya kilimo na masoko haya tutayapata tu iwapo tutafanikiwa katika Serikali ya viwanda. Tutajenga viwanda vya kusindika mahindi, pamba, ufuta, alizeti, tangawizi na kadhalika. Hilo ninaliona hatujalifanyia kazi kwa namna ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, unaona kwamba mahitaji ya mafuta ya kula peke yake ni lita 400,000, hizi ni sawa na alizeti tani milioni mbili tu. Na hizi tani milioni mbili wana uwezo wa kuzalisha wakulima 4,000 tu, wanaweza kuzalisha mafuta yote ya kula…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi hiki, hizi lita za mafuta laki nne wanaweza kuzalisha wakulima 4,000 tu iwapo watajengewa uwezo. Lakini inasikitisha kuona hadi leo asilimia 70 ya mafuta ya kula tunaagiza kutoka nje, wakati wakulima wengi hawana fursa ya kuzalisha na kuuza kwa bei nzuri mazao yao kilimo, kwa hilo ni tatizo. Tatizo hili linatoka wapi...(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzunguzaji)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuhitimisha Hoja ya Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Wabunge 23 walipata nafasi ya kuzungumza. Iingie kwenye kumbukumbu za kudumu za Bunge kwamba hoja hii ni moja katika hoja chache sana ambazo ndani ya Bunge lako zimepata kibali toka pande zote za Wabunge bila kuyumba. Sababu ni kwamba Waheshimiwa Wabunge wote wanaamini kwamba mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, hayawezi kutenganishwa kamwe na mafanikio ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye alihudumu kama Makamu wa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo moja limezungumzwa kwa namna ambayo linahitaji kidogo tulifafanue; hoja ya demokrasia na uhuru wa Habari. Kwamba Mheshimiwa Khatib na baadhi ya Wabunge humu ndani kuweza kuhama kutoka kwenye Chama cha CUF na kwenda ACT Wazalendo na kuweza kushiriki katika Uchaguzi na kushinda na kuzungumza ndani ya Bunge hili ni demokrasia ya kiwango cha juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, demokrasia huanzia ndani ya vyama. Kitendo cha Chama Cha Mapinduzi kuendelea na utaratibu wa kubadilisha wenyeviti wao kila miaka kumi ni kielelezo cha kutosha cha ukomavu wa demokrasia ndani ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeshauri vyama vingine vifuate utaratibu huo kwa sababu huwezi kuwa na legitimacy ya kupigania demekrasia nje kama hujaimarisha demokrasia ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, tafsiri sahihi ya demokrasia; na hapa namnukuu Balozi Dkt. Wilbrod Slaa; demokrasia ya kweli ni demokrasia ya kuwasikiliza na kuwahudumia watu wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wa Tano alifanya kazi hii kwa uaminifu mkubwa akishirikiana na Rais wetu wa sasa, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Kote walikopita Watanzania wamelilia elimu, maji, huduma za afya, mahitaji ya mitaji kwenye biashara na yale yote yaliyowekwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na hayo yote ndiyo yaliyobebwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza kabisa naomba niungene na wewe pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote pamoja na Watanzania kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kukurejesha salama na kuendelea na majukumu yako ya kulijenga Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, naomba kutumia nafasi hii kuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna ambavyo wametupa kipaumbele wananchi wa Madaba. Wizara ya Afya, Maji, Elimu, Miundombinu, Umeme na TAMISEMI hawajakauka katika Jimbo la Madaba. Kwa kweli, katika maeneo hayo tumepiga hatua kubwa sana na wananchi wa Madaba hawataridhi kama nitaanza hotuba yangu bila kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wa Wizara hizo pamoja na watumishi wote wa Wizara hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, sitawatendea haki Mashujaa wa Vita ya Majimaji ambao tunawakumbuka tarehe 27 Februari, kila mwaka kwa sababu nisiposema baadhi ya maneno yamepotoshwa ndani ya Bunge lako Tukufu. Wiki iliyopita Mheshimiwa Ngombale aliilalamikia Serikali kana kwamba makumbusho tunayoyafanya Majimaji ni upendeleo.

Mheshimiwa Spika, tutatafuta nafasi ya kulifafanua, lakini kwa kifupi tu ni kwamba, historia ya makumbusho ya Majimaji sisi wenyewe wakazi wa Mkoa wa Ruvuma tulianza kuchukua hatua kuwakumbuka mashujaa wale na Serikali imekuja kushirikiana na sisi karibu miaka 90 baadaye. Sheria na miongozo ya Serikali ipo, nimshauri tu Mheshimiwa Mbunge afuatilie hatua mbalimbali za kufikia huko na sisi Wanaruvuma tunaunga mkono sana jitihada za Watanzania wenzetu waliopigana vita kulinda heshima ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niende moja kwa moja kwenye hotuba yangu. Hotuba yangu nitaiweka kwenye eneo moja tu kubwa muhimu, juu ya namna gani Serikali ya Tanzania, Serikali ya Uchumi wa Viwanda inahitaji sana ushiriki kamili wa Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki kifupi Wizara hizi mbili, Wizara ya Viwanda na Wizara hii ya Nishati, wamepiga hatua kubwa sana, hatua ambayo Waheshimiwa Wabunge hatuwezi kuibeza. Upande wa viwanda na biashara idadi ya viwanda imeongezeka kutoka 454 ambayo ilikuwa mwaka 2015 na sasa tuna viwanda vipya tu katika kipindi hiki cha miaka mitatu, viwanda 3,306.

Mheshimiwa Spika, katika hili nitaweka nukta kidogo. Kuna watu wanaibeza Serikali wakisema kwamba, viwanda hivi 3,306 si viwanda vyenye hadhi ni mashine za kusaga, sijui mafundi chereheni. Watu wafanye kazi ya kutafuta takwimu. Idadi ya ajira katika kipindi hiki kifupi, kwenye sekta binafsi, sekta ambayo inatokana na viwanda, ilifika 137,054; ukigawanya kwa idadi ya viwanda unapata wastani wa kila kiwanda kimeajiri watu wasiopungua 40. Sasa watu 40,000 si kiwanda? Watu wafanye kazi ya kutafuta takwimu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine kuhusu viwanda tumepiga hatua; mwaka 2015 sekta hii ilikuwa inakua kwa asilimia 7.9 na sasa inakua kwa asilimia 9.8. Huu ni ukuaji mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, sekta ya umeme nayo imepiga hatua ambazo hatuwezi kuzibeza. Moja, sekta hii imejiwekea malengo ya mwaka 2020 ya kuwa na megawatts 4,915 na 2025 megawatts 10,000. Kwa kipindi hiki kifupi kuanzia mwaka 2015 wakati Serikali ya Awamu ya Nne inamaliza kipindi chake cha madaraka, ilimaliza wakati Watanzania tuna umeme wa megawatts 1,308 tu; leo tuna megawatts zaidi ya 2,500. Katika kipindi hiki kifupi katika sekta ya umeme, umeme umeongezeka kwa asilimia 52, hili si jambo la kubeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, Wizara hii inayoshughulika na umeme imeweka mikakati madhubuti ya kufikia malengo ya kuwa na umeme wa megawatts 4,915. Ipo miradi mipya ambayo imeanzwa ikiwepo Stieglers Gorge, lakini unaona kwenye Kinyerezi I na Kinyerezi II tunaona kuna Kinyerezi I Extension ambayo itazalisha umeme wa megawatts karibu 250, lakini kuna Kinyerezi III ambayo itazalisha umeme megawatts 600. Hiyo ni mikakati mizuri itakayotupeleka kwenye malengo yetu ya mwaka 2020.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, naona kuna watu wemesema jimboni kwangu. Nichukue nafasi hii, kwa vile nimekumbushwa niishukuru sana Wizara ya Nishati. Leo katika historia ya Madaba, mwaka huu uliokwisha tarehe 25 Desemba, 2017 wananchi wa Madaba wameanza kupata umeme, tangu kupata uhuru. Hili ni jambo la historia na ni jambo la kujivunia sana, naomba niishukuru Wizara katika kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, sipendi kusema kwamba, kila penye mafanikio hapakosi fitina, lakini nataka niseme kila panye mafanikio hapakosi changamoto. Malengo ya megawatts 4,915 tuliyojiwekea kwa mwaka 2020 na malengo ya megawatts 10,000 tuliyojiwekea ukilinganisha na Tanzania ya uchumi tunaoutaka ni kiwango kidogo sana cha umeme.

Mheshimiwa Spika, nitatoa mifano kadhaa. Zipo nchi kadhaa ambazo zimepiga hatua ambayo sisi sasa tunaelekea, lakini huko nyuma zilifanana sana na sisi kiuchumi na kimikakati.

Mwaka 1970 nchi ya Afrika Kusini ilikuwa na umeme wa megawatts 14,000 sisi leo tuna megawatts 2,500 na tunakwenda kutengeneza Tanzania ya viwanda kwa mkakati wa kuwa na megawatts 4,915. Umeme huu hautoshi kabisa na haya malengo ni ya chini sana, hayatatupa Tanzania ya viwanda tunayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ipo mifano mingi. Mexico mwaka 1994 walikuwa na megawatts 35,000; lakini leo Afrika Kusini wanaongelea megawatts 44,000 wakati nchi nyingine kama za Korea Kusini wanaongelea megawatts 84,000 sisi tumejiwekea malengo ya megawatts 4,000. Pamoja na kupiga hatua kubwa katika hilo, lazima tukiri kwamba, mkakati wetu lazima tuubadilishe na lazima tutengeneze vipaumbele.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka niishauri Serikali kwenye eneo hili. Natambua mikakati mikubwa ambayo Serikali imejiwekea kwenye umeme, tuna mikakati hiyo ambayo nilikwishaitaja. Hata hivyo, kadri ya utafiti wa Benki ya Maendeleo ya Afrika vyanzo vya umeme wa Tanzania vinavyotokana na maji haviwezi kutupatia umeme unaozidi megawatts 4,000. Tunataka tutafute megawatts 10,000 na tunataka tufike megawatts zaidi ya 40,000 ili kupata Tanzania ya viwanda. Hiki kiwango ni kidogo, ni lazima Serikali iangalie vyanzo vingine.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba zilizotangulia tumeongelea kuhusu umeme wa gesi, nadhani kwa bahati mbaya Mheshimiwa Waziri Mkuu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi asubuhi ya leo ya kuchangia sekta muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa. Kwanza kabisa, niwapongeze Wizara na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kusimamia vizuri sana sekta hii ya viwanda na biashara kiasi kwamba wadau tunapata matumaini kwamba tunaweza kuifikia Tanzania ya viwanda ndani ya kipindi chake cha miaka 10 ya uongozi wake mahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huwezi kupata Tanzania ya viwanda kama tutaendelea kupuuza mradi wa Liganga na Mchuchuma. Mradi huu wa Liganga na Mchuchuma, nataka nitumie nafasi hii nieleze vizuri, ulianza kuzungumziwa na Mbunge mtangulizi wa Mheshimiwa Jenista Mhagama, Mheshimiwa Prof. Simon Mbilinyi, lakini imekuja kuongelewa kwa zaidi ya miaka 10 na Mheshimiwa Jenista Mhagama (Waziri) na mimi ni Mbunge wa tatu kulizungumza hili lakini mpaka leo commitment ya Serikali imekuwa ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Liganga kuna chuma, tathmini inaonesha chuma iliyopo Liganga inaweza kuchimbwa kwa kiwango cha tani milioni moja kwa mwaka, hiyo ni tani ya chuma. Chuma hii pamoja na kuzalisha chuma, inazalisha mazao mengine yanayoambatana na chuma. Kuna madini ya vanadium pentoxide na kuna titanium dioxide, haya nayo ni madini yanayoambatana na chuma. Watanzania wote tunajua chuma ni malighafi ya msingi ya viwanda. Ujenzi wa viwanda unatumia sehemu kubwa chuma, mashine zote za viwandani kwa asilimia kubwa zinahitaji chuma, unaipataje Tanzania ya viwanda bila kuchimba chuma ya Liganga? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda jikoni utakuta kijiko, kisu, na uma, hivi vyote vinatengenezwa na chuma. Ukienda shambani utakuta jembe, panga, nyundo, vinatengenezwa na chuma. Ukipanda gari, asilimia 80 ya gari ni chuma, ni utajiri mkubwa sana Watanzania tumeauacha pale Liganga. Ipo mifano mingi, tukienda kwenye nyumba zetu tunazozijenga, bati ni product ya chuma, madirisha yetu, nondo na grill zote hizi ni product ya chuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni viwanda vingapi vinaweza kuanzishwa kutokana na chuma ya Liganga? Tunaweza kutengeneza viwanda vya bati, viwanda vya nondo, viwanda vya magari na kila aina ya kiwanda tunachokitaka tutatengeneza na sisi wenyewe tutakuwa wateja namba moja wa hivyo viwanda. Hatuwezi kuipata Tanzania ya viwanda kama hatuweki makusudi kwenda kuchimba chuma ya Liganga.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1864, nchi ya Marekani iliahirisha ujenzi wa reli kwa sababu walitaka watumie chuma yao kujenga reli kwa sababu waliamini kiwango cha chuma ambacho kitahitajika kujenga reli iwapo kitachimbwa ndani ya nchi husika, kwanza kitaokoa pesa kubwa ya Serikali lakini kitachangia sana kwenye pato la Taifa. Mwaka ule 1864 wakati Marekani wanajenga reli chuma cha ndani kilikuwa na bei mara mbili ya chuma kilichokuwa kinatoka nje ya nchi ya Marekani, hata hivi kwa sababu ya uzalendo waliamua kutumia chuma iliyozalishwa ndani. Kwenye hili niombe sana Wizara iamue sasa kwenda kuchimba chuma cha Liganga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, chuma cha Liganga pamoja na kutoa malighafi ya tani milioni moja ya chuma kwa mwaka itatoa ajira takriban 4,000. Ajira 4,000 ni mchango mkubwa sana kwenye idadi ya ajira. Tumesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ni nzuri. Hata hivyo, ukifanya uchambuzi, ajira zilizozalishwa kati ya mwaka 2015 mpaka 2017 ni 26,113, ajira 4,000 zina mchango gani katika hiyo maana yake ni zaidi ya robo ya ajira zilizozalishwa katika kipindi hicho.

TAARIFA . . .

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa mikono miwili taarifa hii. Nikibaki hapo, ajira zitakazozalishwa kwenye mgodi huu wa chuma pamoja na spillover effect, maana yake ni zaidi ya ajira zilizozalishwa katika kipindi hiki chote cha utawala huu, kwa hiyo, si jambo la kulifanyia dhihaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nabaki hapo hapo kwenye Liganga na Mchuchuma, mradi wa Mchuchuma utakaozalisha kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe, umeme ambao utazalishia chuma cha Liganga, mtambo huu utakuwa na uwezo wa kuzalisha umeme megawatts 600, hiyo ni faida nyingine. Sasa megawatts 600 ni sawasawa na nusu ya umeme wote tuliokuwa nao mwaka 2015. Mheshimiwa Rais amekabidhiwa nchi hii ilikuwa na umeme wa megawatts 1,308 sasa Mchuchuma peke yake itazalisha umeme megawatts 600, si kitu kidogo wala siyo cha kukidharau. Umeme huu sawa na robo ya umeme wote utakaozalishwa kwenye Stiegler’s Gorge. Stiegler’s Gorge watazalisha umeme megawatts 2,100 na megawatts 600 ni robo ya huo umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisisitize kwa kusema umeme huu wa megawatts 600 utakaozalishwa Mchuchuma ni asilimia
12.2 ya malengo tuliyojiwekea ya umeme tunaohitaji mpaka ifikapo mwaka 2020. Sasa unajua huwezi kuipata Tanzania ya viwanda bila umeme. Katika michango yangu iliyotangulia nilisema, umeme tulionao Tanzania hauwezi kutupa Tanzania ya viwanda. Afrika Kusini mwaka 1970 walikuwa na megawatts 14,000, sisi leo tuna megawatts 1,500 mpaka 2,500, tunahitaji uzalishaji mkubwa wa umeme. Mradi wa Stiegler’s Gorge ni mradi muhimu sana kwa Taifa letu, lazima tuupe nguvu, lazima tuunge mkono lakini lazima tuongeze vyanzo, chanzo kingine ni huu wa Mchuchuma, megawatts 600, kwa kutumia makaa ya mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeongea kwa msisitizo mkubwa kwa sababu ninaamini hatuwezi kuipata Tanzania ya viwanda bila umeme wa kutosha na hatuwezi kuipata Tanzania ya viwanda bila kwenda Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Spika, niongezee tu hapo, kwenye hili suala la umeme. Wenzetu nchi nyingine wanaongea megawatts 84,000 sisi tunaitafuta Tanzania ya viwanda bila kwenda kuchimba chuma, bila kwenda kushughulika na Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine nichangie tu kwamba, Tanzania tuna bahati, tumeendelea kuvutia wawekezaji na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri amefanya sana kazi tumeona wawekezaji toka nchi mbalimbali wanakuja kutoka Ujerumani, Ufaransa, ni initiative kubwa sana hii, watu wamebeza lakini wanabeza kwa sababu hawajui misingi ya uchumi. Hawa wanapokuja watatuongezea teknolojia na mtaji, tutahakikisha kwa kuwatumia hao tunavuka, tunafikia haya malengo yetu lakini eneo muhimu ni kulinda viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu muda haujanitosha, nichukue nafasi hii kukushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye hoja na mchango wangu utajikita kwenye eneo la soko la mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kupata mapinduzi ya kilimo Tanzania kama hakutakuwa na mfumo madhubuti wa soko la mazao. Kinachomfanya mwananchi wa Madaba, mwananchi wa Njombe, Songea Mkoa wa Ruvuma, mwananchi wa Katavi, mwananchi wa Rukwa, mwananchi wa Sumbawanga, Songwe na Mbeya aamke asubuhi, aweke jembe begani akalime ni kwa sababu anataka kupata pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima haendi kulima kwa ajili ya kutatua tatizo la food security ya nchi, ile ndiyo ofisi yake. Mwananchi wa Madaba, mwananchi wa Katavi anakwenda kulima mahindi kwa sababu anataka ajenge nyumba bora, kwa sababu anataka asomeshe mtoto wake katika shule zenye sifa, kwa sababu anataka amudu mahitaji ya afya katika hospitali zenye ubora, anataka kuishi maisha bora huyu Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaongelea asilimia 70 ya Watanzania ambao kipato chao kinatokana moja kwa moja na shughuli za kilimo, lakini tunaongelea asilimia karibu 90 ya Watanzania ambao kwa namna moja au nyingine wanategemea kilimo. Huwezi kupata mapinduzi ya kilimo bila mfumo madhubuti wa soko la mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Madaba wameumia sana na mfumo wa masoko, pia wananchi wa Mikoa yote niliyoitaja ukiwemo na Morogoro wameumia sana juu ya ukosefu wa soko la mahindi. Wakulima hawa kama ambavyo Wabunge tunataka tuwasomeshe watoto wetu katika shule zenye sifa, tujitibu vizuri, tujenge nyumba bora, tuvae nguo safi, nao pia wana ndoto hiyo. Hatuwezi kuipata Tanzania yenye mapinduzi ya kilimo kama hatutaki kuwekeza kwenye masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe ushahidi, ukuaji wa sekta ya kilimo mwaka 2014/2015 ulikuwa asilimia 3.4 na ukuaji wa sekta hiyo mwaka jana 2016/2017 ilikuwa asilimia 2.1, kwa nini? Kwa nini ukuaji umeshuka ni kwa sababu incentive ya mkulima ni soko. Hawezi kwenda kununua mbolea, hawezi kujikita kwenye mbegu bora, hawezi kutafuta mbinu bora za kilimo kama kilimo hakimlipi. Kwani ni nani ameenda kuwaambia vijana wanunue bodaboda, wafanye biashara Mjini, si kwa sababu inalipa? Hivi leo tunahitaji kuwambia wakulima wakalime? Tuwape soko wakulima watakwenda kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima yeyote akishajua tangawizi inamlipa, mahindi yanamlipa, kahawa inamlipa huhitaji kwenda kumfundisha kulima atakutafuta mwenyewe, atakuambia nifundishe namna ya kulima mahindi, atakutafuta mwenyewe atakuuliza umwambie mbolea iko wapi. Leo tunawaweka wananchi wetu wakulima katika mazingira magumu sana, Madaba na maeneo mengine masikitiko ni makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea na hoja yangu nimshukuru sana Waziri na Ofisi yake Wizara ya Kilimo wamenisaidia sana, mwaka huu nilikuwa napoteza Ubunge Mabada kama suala la mbolea lisingezingatiwa. Ucheleweshaji ulikuwa mkubwa, wananchi wamelalamika lakini nakushukuru Waziri ulinisaidia na timu yako ya Katibu Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la soko la mahindi Serikali inajaribu kulitatua lakini bado halijapatiwa ufumbuzi. Mwaka 2015/2016 tulikuwa na ziada ya tani milioni 2.6 Serikali ilinunua tani 22,000 tu, mwaka uliofuata tani milioni tatu ziada Serikali ilinumnua tani 62,000 tu za mahindi. Mkoa wa Ruvuma hapa nina taarifa aliyopewa Waziri Mkuu alipokuja, tulizalisha ziada ya mahindi/nafaka tani milioni 1.4, ilinunuliwa tani 10,000 tu, tunakwenda wapi? Wakulima hawa wote mahindi haya wameyapeleka wapi? yameharibika, wameendelea kuwa maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya kuzingatia muda nitakwenda moja kwa moja kwenye ushauri. Mheshimiwa Waziri azingatie mambo yafuatayo:-

Moja, sera ya kilimo inataka mambo manne nchi yoyote, nenda Marekani, nenda nchi zozote za Kusini mwa Afrika, Kenya na kokote sera yoyote ya kilimo ina mambo manne ambayo ni safety, security, sufficiency na quality ya maisha ya mkulima. Mheshimiwa Dkt. Tizeba hili naamini unalizingatia na tunaomba sana ulizingatie. (Makofi)

Pili, sera yoyote ya agricultural trade, sheria zote za mipakani zilenge kulinda maslahi na maendeleo ya wakulima ndani ya nchi yako ndipo utapata haya yote unayotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda haraka haraka. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imetoa mapendekezo juu ya ufumbuzi wa tatizo la soko la mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja imesema katika ukurasa wa 12, tuanzishe soko la mazao sasa commodity exchange kwa maana ya kwamba wakulima wetu wanapoingia shambani wawe na uhakika wa soko. Leo Sudan hawana chakula, Uganda na Tanzania tunapishana misimu ya kulima, Kenya wanahitaji mahindi ya Tanzania leo tunasema tunawanyima mahindi wakati mahindi yanaoza Madaba. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imetoa muongozo kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili imependekeza NFRA iwe na kitengo cha kununua mahindi, inunue mahindi ya hifadhi lakini inunue mahindi ya kutosha kwa ajili ya kutafuta soko la nje. Kama tunataka ku-control inflation, kama tunataka tu-control food security basi NFRA apewe hayo majukumu, leo amepewa bilioni 15 badala ya kupewa shilingi bilioni 86, shilingi bilioni 15…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kukushukuru kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango ya Taifa 2019/2020. (Makofi)

Kwanza nimpongeze kwanza Mheshimiwa Waziri Mpango na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na Serikali ya Awamu ya Tano, katika ujumla wake kwa kuwa consistency katika kipindi hiki chote cha miaka mitatu kwa sababu mpango huu ni sehemu ya mpango mzima wa miaka mitano 2015/2016 - 2020/2021 na katika utekelezaji wake Serikali imekuwa consistency sana.

Pia niipongeze Serikali kwa kuzingatia maoni ya Wabunge kwa miaka yote mitatu ambapo tumekuwa tunatekeleza mpano huu. Maeneo kadhaa ambayo tulikuwa tunashauri yakiwemo maeneo ya kuongeza nishati tumeona Stiegler’s Gorge imeendelea kupewa kipaumbele lazima tuipongeze lakini pia tumeona leo Liganga na Mchuchuma, inaanza kupata sura ya utekelezaji kwa maana kwenda sasa kujenga kiwanda cha kufua chuma Liganga. Sasa haya yote ni mapato ya kazi ya Bunge hili na nimatokeo ya kazi nzuri ya Awamu ya Tano, na lazima tuipongeze Serikali na kwa namna ya pekee Mheshimiwa Rais na Waziri Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la kukua kwa uchumi wote tumejiridhisha pasipo mashaka uchumi wetu unakua kwa kasi kubwa sana na ukilinganisha na uchumi unavyokuwa duniani na uchumi unavyokuwa katika Afrika na maeneo mengine tunayopakana nayo sisi tunakuwa kwa kasi kubwa sana, kasi ya asilimia 7.2.

Sasa hili kimsingi kuna eneo dogo linatupa shida kidogo sisi Wabunge lakini Watanzania katika ujumla wake kwamba uchumi unakua, lakini mapato ya kukuwa uchumi huu tunayaona kwenye maeneo ya afya, tunaona kwenye masuala ya elimu, tunaona kwenye masuala ya miundombinu. Kwa hiyo, kimsingi faida za kukua uchumi huu tunaziona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambayo mimi nilitaka nitoe mapendekezo, ya kuboresha wakati wa maandalizi ya huu mpango ni namna gani sasa kwa sababu mimi nina amini hatuwezi kupata mapinduzi ya uchumi kama hatutakuwa na mapinduzi ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilitaka nijaribu kushauri kwamba sasa Mheshimiwa Mpango akae na hizi line ministry zinazogusa sekta ya kilimo na uchumi kiujumla kuona namna gani sasa tunaweza ku-transform agricultural sector kwa namna ni significant. Waatalam wa kilimo wanapo taka kujua changamoto kwenye sekta ya kilimo wanafanya upembuzi wa mnyororo wa thamani ya mazao ya kilimo na ukifanya upembuzi wa mnyororo wa thamani wa mazao ya kilimo katika ujumla wake utagundua kwamba tatizo kubwa kwenye sekta ya kilimo ni soko, yaani huo ndiyo mtego tunao na Serikali sasa lazima ikubali kwamba huo ndiyo mtego ambao tunao na tukiweza kuutegua huo sekta ya kilimo itakuwa kwa kasi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye huu mpango nashukuru Serikali imeweka vizuri sana interventions nyingi kwenye sekta ya kilimo, lakini utaona kwenye interventions zilizopendekezwa na Serikali kwenye mpango huu hazioneshi kwa ufasaha namna gani tunaenda tunaenda kutatua tatizo la soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachomfanya mkulima aende shambani ni faida anayoipata kutokana na kilimo. Tumejiridhisha kwamba kwa namna yoyote ile kwa mazingira aliyopo mkulima huyu mdogo lazima achangie kwenye usalama wa chakula, lakini lazima atengeneze fedha kwa ajili ya kujikimu. Sasa strategy ya Serikali lazima izingatie ukweli kwamba kumsaidia huyu mkulima mdogo apunguze gharama za uzalishaji na gharama za uzalishaji kwanza zinatokana na bei kubwa ya mbolea, nashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu jana alieleza namna gani tunajipanga kupunguza gharama ya mbolea kwa kuzalisha mbolea yetu ndani, hilo litamaliza tatizo lakini kwenye mpango huu alijafafanuliwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili ni transaction cost kutoka eneo lile ulilozalisha mpaka kufika kwenye maghala ya kuhifadhia mazao, barabara zetu vijijini hazileti tija kwa mzalishaji, eneo dogo la usafirishaji analipa gharama kubwa sana za kusafirisha mazao yake,
anapofikisha zao lake kwenye eneo la soko tayari garama imeshakuwa kubwa. Kwa hiyo anapokutana na bei ndogo, profit margin inabaki kuwa ndogo sana au anaweza asiipate kabisa. Kwa hiyo, Serikali iwekeze kwenye kupunguza gharama za uzalishaji kwa kupitia pembejeo zetu, mbegu bora na mbolea, lakini pia miundombinu ya masoko, na miundombinu ya masoko ndiyo hizo barabara za vijijini zinatoka mashambani lakini madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine baya linalochangia upotevu mkubwa wa mazao tunasema post harvet losses ni haya hadhi na sura ya maghala yetu na gharama za usafirishaji (miundombinu ya usafirishaji) asilimia 30 ya mazao yetu tunayoyazalisha yanapotea kabla hayajafika kwenye soko, sasa hiki kiwango kinacho potea nacho ni hasara kwa mkulima. Kwa hiyo pamoja kwamba hatuwezi kumsaidia mkulima kupata bei nzuri kutokana na hali halisi ya soko la dunia tunaweza kama Serikali kumwezesha huyu kuzalisha kwa gharama za chini na hii profit margin yake ikabaki kubwa na akawa ana visenti vya kwenda shambani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliomba nimshauri Mheshimiwa Mpango na Serikali katika ujumla wake katika eneo hilo na ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu sana kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Awali ya yote naomba nitumie nafasi hii kuwashuru na kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Madaba kwa kuitikia wito wa Mheshimiwa Rais wa Hapa Kazi Tu kwa vitendo. Wameshiriki kikamilifu katika ujenzi wa miundombinu ya elimu yakiwemo madarasa, mabweni na mabwalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee niwapongeze wananchi wa vijiji vya Wino, Lilondo na Maweso ambao katika umoja wao wamechangia zaidi shilingi milioni 104 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba makazi yao yanapata maji lakini shule zote za sekondari na za msingi wanapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti niwapongeze wazazi wa shule zote za msingi za Madaba. Kwa namna ya pekee, wazazi wa Shule ya Msingi Njegea, Igawisenga, Turiani, Kifaguro, Mahahanje, Likalangilo na shule nyingine ambazo katika umoja wao katika kila mwaka wanachangishana zaidi ya shilingi milioni 10 kwa ajili ya kupata walimu wa ziada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali na kwa namna ya pekee Wizara hii ya Elimu na TAMISEMI ambao wameunga mkono jitihada za wananchi wa Madaba kwa kuhakikisha kwamba ile miundombinu ambayo wazazi wameendela kuijenga, Serikali inaikamisha. Tumepata fedha nyingi kwa ajili kukamilisha, lakini kutokana wingi wa mahitaji yetu, bado hizo fedha hizo hazitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sikupata nafasi kuchangia kwenye Wizara ya TAMISEMI, nitumie nafasi hii hii pia kuiomba Wizara ya TAMISEMI watuongee bajeti na kuhakikisha kwamba madarasa, mabweni na mabwalo ya shule zetu za msingi na sekondari yanakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekti baada ya hizo shukrani kwa wananchi wa Madaba na kwa Wizara, nitumie nafasi hii kutoa wito kwa Wanamadaba kuhakikisha kwamba tunaendelea kuunganisha nguvu zetu kwa pamoja kwa sababu tuna jukumu la pamoja kuhakikisha kwamba watoto wetu wanapata elimu bora na wanapata katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nitoe ushauri kwa Serikali. Tunayo changamoto kubwa sana ya walimu katika shule zetu. Hili siyo kwa Shule za Madaba pekee, ni shule za sekondari karibu taifa zima. Tatizo hili la walimu pengine tunaweza tukalichukua kama dogo, lakini madhara yake yanaonekana dhahiri katika maeneo tunayotoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna vijana waliohitimu kidato cha nne katika shule zetu mbalimbali. Kijana huyu tangu anaanza Form One mpaka anamaliza kidato cha nne, kwa sababu ya kukosa Walimu darasani, wametumia madarasa yetu kama vijiwe vya kujadili masuala ya siasa na kuijadili Serikali katika mambo wasiyoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wanapotoka mashuleni wanahamishia mijadala kwenye vijiwe na kwenye mitaa yetu. Kwa kadri tunavyoendelea, Taifa hili sasa linaelekea kupata wanung’unikaji na siyo watenda kazi katika Taifa hili. Jambo hili leo tunaweza kulichukulia mzaha mzaha, lakini kwa kadri siku zinavyokwenda, tunazalisha vijana wa kijiweni ambao hawana ajenda nyingine zaidi ya kulalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia imeelezwa kuhusu sera yetu ya elimu. Nimeona Wizara imeweka mkakati wa ku- review hii sera sayansi, teknojia na ubunifu. Hili lisichukue muda. Mwaka 2018 tumeona huo mchakato ukiangalia kwenye hii taarifa ya Wizara ambayo ni nzuri sana, lakini unaona katika ukurasa wa tisa wanasema Wizara imeanda Rasimu ya Mapitio ya Sera ya Sayansi Teknolojia na Ubunifu. Mwaka umeisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa bajeti Wizara inaendelea na mchakato na inasema itakamilisha Mapitio ya Sera ya Sayansi na Teknolojia ya Mwaka 1996 ili kuwa na Sera ya Sayansi Teknolojia na Ubunifu inayoendana na mahitaji ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa miaka miwili inakatika; hili haliakisi kabisa kasi ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Naiomba Wizara Watanzania wanatambua umuhimu na wanaona jithada zinazofanyika na hawana tatizo, lakini tuongeze speed ya kufanya kazi. Tufanye review ya hii sera kwa wakati ili Watanzania waliopo mashuleni, waliopo kwenye vyuo vyetu za ufundi waweze kunufaika na hii sera. Tutaisubiri hadi lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini sera hii inayoenda kufanyiwa review itazingatia ukweli kwamba kila Halmashauri ya Wilaya tunahitaji kuwa na Vyuo vya Ufundi na siyo kimoja. Kwa sababu watoto wanaohitimu kidato cha nne ni wengi, wanaopata fursa ya kujiendeleza sekondari kwa maana ya kidato cha tano na cha sita na wanaokwenda Vyuo Vikuu ni wachache. Hawa wanaobaki tunawaachia ujuzi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini hatutaki ku- capture? Kwa nini hatuataki ku-tap hii rasilimali muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu? Namna nzuri ya kutumia hii rasilimali watu ambayo ina ari ya kazi ni kuiongezea ujuzi kupitia vyuo vyetu vya elimu. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri tuwajengee uwezo vijana wetu wawe na uwezo wa kiufundi na kiujasiliamali ili tuondoe tabia yao ya kulalamika, tuwajenge uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, walimu wetu katika maeneo mbalimbali wana hali ngumu sana. Wengi hawajapandishwa madaraja kwa muda mrefu. Kwa hili sisi Wabunge tumetekeleza wajibu wetu wa kuja mpaka kwenye Wizara zinazohusika kuyaeleza, lakini hayafanyiwi kazi. Wengine madaraja yamekwama kwa miaka minne, mitano; wengine posho zao za miaka mingi tunakwenda kujenga Taifa la walimu wanaolalamika ambao watawazaa wanafunzi na vijana wanaolalamika na mwisho tutapata Taifa la walalamikaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu sana Wizara ya Maji, na nianze kwa kumshukuru sana kuishukuru sana Serikali hususani Mheshimiwa Prof. Mbarawa Makame pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Jumaa Aweso kwa ushirikiano mkubwa sana ambao mmetupa wana Madaba kuhakikisha miradi yetu ya maji inafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Prof. Mbarawa na Mheshimiwa Jumaa Aweso mmekuja wenyewe mmetembelea miradi mbalimbali ya maji Madaba, mmeshirikiana na wananchi wa Lilondo kuhakikisha kwamba miradi yao ya jamii kupitia vikundi inafanikiwa kwa kuchangia pesa ninyi wenyewe, pia kwa kuwatia moyo ninawashukuruni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishukuru miradi mingine ambayo inaendelea iliyokamilika Madaba ya maji na hii ambayo imetengewa bajeti ya zaidi ya bilioni moja kwa ajili ya kuendelea kuitekeleza. Siku ya leo nilitamani sana nitume muda mrefu kuishauri Serikali juu ya mambo kadhaa ambayo ninadhani kama hayatachukuliwa umaanani Wizara hii itawaangusha watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza naomba tulijue kwamba kama vitu ambavyo vinambeba Mheshimiwa Rais ni uzalendo wake na upendo wake kwa watanzania. Amejitoa kwa hali na mali kufa na kupona Watanzania wapate unafuu katika Nyanja zote, amekusudia kwa kufa, kupona kuhakikisha wakina Mama tunawatua ndoo vichwani ili kuhakikisha hawapati tena usumbufu wa maji. Lakini Watumishi ndani ya Wizara ya Maji ni mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie kusema na hili limesemwa na Mheshimiwa Waziri mwenyewe kwenye ukurasa wa 108 wa hotuba yake. Amesema: “moja katika changamoto katika Wizara hii ni uwezo mdogo katika utekelezaji, usimamizi na uendeshaji wa miradi ya maji” na kama ningepata fursa ya kurekebisha hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ningeiandika kama ifuatavyo: “Dhamira ndogo ya Watumishi katika idara inayohusiana na masuala ya maji kutekeleza na kusimamia miradi vizuri”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa nyingi zimetengwa kwenda kwenye miradi, sisi Madaba pia tumetengewa na Mheshimiwa Waziri anahangaika sana kuhakikisha tunafanikiwa, lakini procedure ndogo tu ya kupata vibali vya kutekeleza miradi iliyotengewa fedha inachukua karne nzima. Mwaka mzima Mtumishi wa Madaba anaandika barua Wizarani, anasubiri majibu ya kibali cha kutekeleza mradi. Mradi umetengewa fedha, tupo ndani ya bajeti, mradi hauchukuliwi umaanani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri Mheshimiwa Waziri, watu kama hawa awaondoe, wanamchafua, wanaichafua Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Inawezekanaje wewe umeandikiwa barua Mwezi wa nane, Mtumishi umeipokea kutoka kwa mtaalam mwenzako, hata ku-acknowledge kwamba umeipata hiyo barua na hata baada ya kukumbushwa, inakaa miezi sita, saba mpaka Mbunge anakwenda kwa Waziri, Waziri anafuatlia ile barua, tutafika kweli na Awamu hii ya Tano? Inasikitisha sana kuona kasi ya Mheshimiwa Rais, kasi ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu Waziri wake inaangushwa na watu wadogo, watu walio katika utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tumebadilika sana, Watanzania tumeakisi falsafa, tumeiishi falsafa ya Mheshimiwa Rais ya “hapa kazi tu”, wananchi wanahangaika kila siku, wanapambana kuhakikisha kwamba tunaitekeleza lakini bado baadhi ya watumishi wa umma wanaishi maisha yale yale ya business as usual. Yamesemwa haya na Mheshimiwa Adadi humu humu ndani, yamesemwa na Mheshimiwa senator hapa, yamesemwa na Mheshimiwa Keissy na mimi nayasema na naamini Wabunge wengine watayasema, wanaotuangusha naomba Mheshimiwa Waziri wa Maji akafanye nao kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto ya certificate, siyo Madaba peke yake, sehemu nyingi tunalalamika sana, Wakandarasi wametekeleza wajibu wao, walipwe ili kazi ziende, lakini nalo hilo linamhitaji Mbunge aende mguu kwa mguu mpaka Wizarani, hawa watumishi wana kazi gani?. Hili kwa kweli limenisikitisha na nimeungana na Wabunge wenzangu kulisema na naamini Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo sisi tunamwamini na tunamtegemea, atakapopitisha Bajeti yake ambayo tutaiunga mkono, aende akasafishe huko chini wanatuangusha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, pamoja na michakato hii, vijiji saba vya Wilaya ya Madaba vimeendelea na utaratibu wa usanifu wa mradi. Mradi wa Vijiji Saba unakwenda kunufaisha wananchi 25,000. Mradi huu ngazi ya Halmashauri walishamaliza usanifu wa awali kabisa na wameomba kwa Mheshimiwa Waziri na amewakubalia, amewapa kibali lakini wameomba pia kwake kibali alichowapa ni kwa ajili ya kuweka maji ya muda mfupi kwa kutumia visima virefu. Tunamshukuru na tunaamini utaanza kutekelezwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo walilonalo ni kwamba wanashindwa kufanya usanifu wa kina kwa sababu zaidi ya miezi sita sasa wanasubiri majibu ya Wizara, waletewe wataalam kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina na pengine hili lingekuwa limeshafanyika leo tungeweza kuisoma Bajeti ya eneo hilo. Mheshimiwa Waziri tunamwomba sana, tunamwamini, tunamtegemea na tunaunga mkono hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Waziri wote wawili kwa ushirikiano ambao wanatupa wananchi wa Madaba kwenye masuala yote ya barabara na mawasiliano na nitoe salam za pekee kutoka kwa wananchi wa Ifinga ambao tangu nchi hii ipate uhuru hawakuwa na mawasiliano kabisa, walikuwa wanasafiri zaidi ya kilomita 30 kwenda kupiga simu, lakini sasa tatizo hilo limekwisha, tunawashukuru sana. Pia watu wa Madaba wanamkumbuka sana Mheshimiwa Waziri, alianza utumishi Madaba na leo ameshirikiria Wizara muhimu sana katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiifuatilia historia ya Madaba utagundua kwa nini ina matatizo makubwa ya barabara, Madaba ilikuwa ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Songea miaka minne iliyopita. Katika kipindi hicho, barabara ambayo ilikuwa inahudumiwa na Serikali kwa kupitia fedha za halmashauri ilikuwa kilometa 48 tu na sasa Madaba ni Halmashauri ya Wilaya na ni Jimbo na kilometa zinazohitaji kuhudumiwa kwa maana ya mtandao wa barabara Madaba umefikia kilomita 642. Mpaka sasa bajeti tunayopata Madaba kwa kupitia TARURA ni ya kilometa 48 tu, haizidi shilingi milioni 400.16. Madhara yake barabara nyingi za Madaba ni mbovu hazifai na hazipitiki katika kipindi cha masika na hata kiangazi bado kuna makorongo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo barabara za kimkakati ambazo naamini Mheshimiwa Waziri tumeanza kuzungumza kwenye vikao vyetu ambavyo siyo rasmi na yeye, lakini hapa naongea mbele ya Bunge hili Tukufu kumwomba akubali kupokea baadhi ya barabara zitoke TARURA ziende TANROADS. Moja katika barabara hizi ni hii barabara ya kutoka Wino kwenda Matumbi – Ifinga. Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Ruvuma na Mkoa wa Morogoro na barabara hii ndiyo barabara ambayo itachangia sana kwenye kuipata Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza hekta za ardhi zimewekeza kule kwa ajili ya kilimo cha miti na muda si mrefu kama Mheshimiwa Waziri atatusaidia, hawa watani zangu wa Iringa tutawapita kiuchumi. Uchumi wetu utafafana na uchumi unaouona Mafinga leo kwa kutokana na miti, lakini kinachotuangusha ni hii barabara. Hii ni barabara ya kimkakati, ni barabara yenye uchumi mkubwa sana. Barabara hii ina urefu wa kilomita 57, pia inaunganisha na mbuga ya Selou ambako tayari kuna vitalu ambavyo wawekezaji wamewekeza kwenye kuwinda na kwenye utalii. Kwa hiyo ina mchango mkubwa sana kwenye uchumi na hatuwezi wana Madaba kushiriki kwenye uchumi wa viwanda kama barabara hii Mheshimiwa Waziri hatakubali kuipokea. Namwomba sana kwa niaba ya wananchi wa Ifinga akubali kuichukua barabara hii iende TANROADS ili ijengwe kwenye viwango tunavyovitaka na matokeo yake ni uchumi ambao utatokana na kazi kumbwa inayofanyika katika maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ukiangalia kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri aghalabu utakuta mahali pameandikwa Madaba, najua kwa sababu labda Madaba barabara zake ni fupi na ni barabara ambazo wanadhani TARURA itazikamilisha, lakini kiuhalisia sivyo hivyo, TARURA hawana fedha za kuweza kumaliza zile barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo barabara nyingine ya kimkakati inayounganisha Madaba na Njombe kwa kupitia Kijiji cha Maweso na kama Mheshimiwa Waziri alifanya kazi Madaba wakati ule, ili uje Dar es Salaam ilikuwa unapita Maweso unaenda Mikongo unatokea Kifanya unakwenda Njombe, ile barabara ya zamani, barabara kubwa ya kutoka Dar es Salaam kwenda Madaba, kwa sasa unaweza kwenda mwisho Maweso, baada ya pale huwezi kuendelea na ile barabara. Namwomba Mheshimiwa Waziri barabara hii pia aichukuwe kwa maana ya Mfuko wa TANROADS aihudumie ili kukuza uchumi wa wananchi wa Madaba na wananchi wa Maweso, lakini wananchi wa Njombe kwa sababu hilo ndilo eneo kubwa ambalo lina ardhi kubwa ya uzalishaji, lakini pia lina matukio ya kihistoria. Barabara hii ina kumbukumbu za kudumu za mashujaa wa vita ya Uganda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mhagama muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Makatibu Wakuu wa Wizara hii wote wawili pamoja na Wakurugenzi kwenye Wizara hii. Mimi nimefanya kazi nao na nime-interact nao, watu hawa ni watu makini sana na iwapo Bunge lako litawashauri vizuri, tutapata mapinduzi makubwa sana kwenye sekta hii, hiyo ndiyo imani yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo sikupenda nichangie kwa sababu ya mazingira yalivyo na mfumo na muundo wa Wizara hii bado haunishawishi kwamba maoni yetu yanaweza kuzaa matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye mapori yote ya Mikoa ya Rukwa, Ruvuma, Tabora, Katavi, mikoa yote ambayo wewe unaifahamu ambayo haikuwa na mifugo, mapori yote yamejaa ng’ombe. Madhara yake ni nini?

Mheshimiwa Spika, madhara yake ni kwamba katika muda mfupi ambao unaweza ukaupima kabisa kwa miaka, Tanzania inakwenda kuwa jangwa; na kwa nini tumefikia hapo? Tumefikia hapo kwa sababu wafugaji wetu kwanza hawana ardhi ya kufugia; lakini pili, hakuna malisho. Kwa hiyo wanahama, wanasafiri, wanakwenda, wanajaribu kuhangaika; lakini la tatu; ubora wa mifugo yetu ni duni, tunafuga wanyama wengi lakini tija ndogo kwenye ufugaji. Hizo ni baadhi ya sababu ambazo nilitaka nizitaje.

Mheshimiwa Spika, nafasi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kumaliza tatizo hili ni ndogo kwa sababu tatizo la kuhama wafugaji halihusu Wizara ya Mifugo peke yake na ndiyo maana nilikuwa nachelea kushauri Bunge lako liishauri Serikali iunde tume au iunde coordination team ambayo itahusisha Wizara zisizopungua tano, wafanye pamoja kazi hii ya kuratibu ufugaji nchini.

Mheshimiwa Spika, wafugaji wanahitaji ardhi, wanamuhitaji Waziri wa Ardhi, wanapotaka kuingia kwenye eneo kuna Maliasili, kuna Kilimo, kuna Mazingira, Wizara hizi zote kama hazitaamua kufanya kazi pamoja hatutakuwa na ufugaji bora nchini, tuta-fail tu. (Makofi)

SPIKA: Nakuongezea na Wizara ya Maji.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, na Wizara ya Maji, ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niombe na nashindwa kwenda zaidi, hatuwezi kutoka hapa tulipo. Leo nchi hii inakwenda kuwa jangwa. Mimi ni mfugaji na nina ranchi, ninafuga lakini nikienda Songea Vijijini kila pori wapo wafugaji na ukiwauliza wanasema hatuna pa kufugia, hatuna ardhi.

Mheshimiwa Spika, leo tunashauri kwamba wapewe ranchi za Serikali, well and good, lakini kama hatuwajengei uwezo wa kuzalisha chakula cha mifugo kwa maana ya pastures, uwezo wa kutengeneza visima vya maji, uwezo wa kuzalisha ng’ombe bora, hatutamaliza tatizo hili kwa sababu tutamaliza hizi ranchi za Serikali lakini bado zitakuwa hazitoshi kwa sababu ng’ombe ni wengi sana.

Mheshimiwa Spika, mimi nikuombe na nitashika shilingi baadaye; Serikali ianzishe coordination team ya kuratibu ufugaji nchini. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Kilimo. Kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri kwa kazi nzuri sana wanayoifanya kwenye sekta hii. Pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuwa msaada mkubwa sana kwa wakulima wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kati ya maeneo muhimu sana ambayo nilitaka nichangie kwa maslahi ya muda ni uelewa ambao tunatakiwa wote tuwe nao. Moja, Mheshimiwa Waziri ujue kwamba hakutakuwa na Mapinduzi ya viwanda nchini kama hatutakuwa na Mapinduzi ya kilimo ni kwa sababu asilimia 65 ya malighafi yanayokwenda viwandani yanatoka kwenye kilimo. Pili, hatutakuwa na mapinduzi ya kilimo kama hatutakuwa na mapinduzi kwenye mfumo wa kufikisha pembejeo kwa wakulima wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anafahamu vizuri, wakulima wetu wengi wapo vijijini, na pembejeo za kilimo kwa maana ya mbolea, mbegu bora na viuatilifu vinapatikana mjini. Ili huyu mkulima aweze kuzalisha kwa tija ni lazima atumie mbolea nzuri, mbegu bora na atumie viuatilifu. Kama hivi vyote vinaendelea kupatikana mjini maana yake huyu mkulima mdogo ni lazima asafiri kupata hii huduma, na unamuongezea gharama za uzalishaji. Akishazalisha zao Lake, anakuja kuliuza kwa gharama kubwa kwa sababu anataka kufidia gharama.

Mheshimiwa Spika, mfumo ambao Serikali unaufanya ni mzuri, wa kuhakikisha kwamba vijijini kunakuwa na maduka madogo madogo ya wauza pembejeo. Maduka haya vijijini yatauza mbolea, mbegu bora na viuatilifu.

Mheshimiwa Spika, changamoto tunayoipata kwenye hii sekta ya kilimo ni gharama za kufungua haya maduka vijijini, wajasiliamali wengi vijijini wamejengewa uwezo na uelewa wa umuhimu wa kuuza pembejeo vijijini ili mkulima mdogo aweze kupata huduma kwa karibu.

Mheshimiwa Spika, sasa vyeti vinavyotokana na kupata hicho kibali ni gharama kubwa sana. TOSIC peke yake wanataka 100,000, TFRA wanataka pia fedha lakini TPRA wanataka 320,000, TFDA wanataka 100,000, kabla hujafungua duka la pembejeo kijijini, lazima uwe na shilingi zaidi ya 600,000; hapo hujaweka shelves dukani, hujanunua bidhaa. Sasa mjasiriamali gani wa kijijini atakuja kuwekeza kwenye hii biashara ili kumsaidia mkulima mdogo kupata huduma kwenye sekta hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, ili tupate mapinduzi ya kilimo, Mheshimiwa Waziri azipitie tena hizi tozo na gharama, ikiwezekana aziondoe, kama haiwezekani basi zipunguzwe kwa kiwango ambacho kitamsaidia mjasiliamali mdogo aweze kuwa msaada kwenye hii value chain ya inputs kwa maana ya pembejeo, tusipofanya hivi tutaendelea kuwatesa wakulima na hatutapata majibu. Ninayo mifano halisi, Kigoma peke yake zaidi ya wajasiriamali 159 wamejengewa uwezo lakini wameshindwa kufungua maduka kwa sababu hawajakidhi viwango vya kuwa na vyeti kwa sababu ya gharama.

Mheshimiwa Spika, ukienda Mkoa wa Kagera wakulima 461 wamejengewa uwezo kupitia Shirika la Agra, lakini ni wakulima 139 tu wameweza kulipia gharama hizi na kufungua maduka vijijini, tutapata wapi mapinduzi ya kilimo kama hatutaki kuwekeza kwenye mfumo wa pembejeo.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, na mimi nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii muhimu sana kwa maslahi ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kati ya mwezi Januari, 2021 mpaka Mei, 2022 mafuta ya aina ya petroli yamepanda kwa asilimia 92; ni asilimia kubwa sana; toka shilingi 1,695 mpaka shilingi 3,200 na kitu huo ni mzigo mkubwa sana kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika miezi hii miwili kati ya Aprili na Mei mafuta yamepanda kwa asilimia 21. Kwa hiyo, ukiangalia katika ujumla wake gharama ya maisha kwa Watanzania imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 92 kati ya mwaka jana na sasa na gharama ya maisha kwa Watanzania kati ya mwezi Aprili na Mei imeongezeka kwa asilimia 21. Wananchi wa Madaba kwa sehemu kubwa wanasaga nafaka kwa kutumia dizeli, maisha yao yameongezeka sana gharama, lakini Watanzania wengi vijijini wanatumia diseli kwenye kilimo.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Joseph Mhagama kuna taarifa kutoka kwa Mbunge wa Kinondoni.

T A A R I F A

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nataka kuongeza kwenye hoja yake na nimpe taarifa kwamba gari yangu mimi nilikuwa nikijaza kwa shilingi 250,000 full tank, jana nimelipa shilingi 350,000 na hivyo aweze kuona uzito wa kupanda kwa bei hizi. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Joseph Mhagama, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante naipokea taarifa muhimu sana kwa kujenga na kunogesha hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni ushauri, kwa sababu maelezo mazuri yametolewa na athari za kupanda kwa bei ya mafuta kwa Watanzania zimeelezwa. Mafuta ndiyo usalama wa Taifa letu, mafuta ndio uchumi wa nchi yetu na mafuta ndio ustawi wa jamii ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mazingira ambayo tunaendana na tunasema ni market economy, uchumi huria unapojiendesha intervention ya Serikali ni muhimu sana kwa sababu huwezi kuliacha soko huria liende kiholela. Soko huria siyo soko holela; kwa hiyo intervention ya Serikali kwenye masuala ya fiscal policy na kwenye masuala ya momentary policy ni lazima yafanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na katika mazingira hayo kwa vile umenipa dakika tano tu naomba nitoe ushauri mahsusi. Tunazo tozo ambazo ukizijumlisha, mimi ningeongea mbili tu. Kuna fuel levy na kuna excise duty kwa pamoja zinachangia shilingi 792. Hapo Mheshimiwa Waziri au Serikali iangalie namna gani tutatoka. Tunajua umuhimu wa tozo zinazohusu ujenzi wa barabara vinakwenda kwa ajili ya ujenzi wa barabara vijijini. Tunajua umuhimu wa tozo zinazotumika kujenga miradi ya maji hizo zibaki kwa sababu tunaenda kuleta maendeleo kwa wananchi. Lakini zipo tozo zingine ambazo tuweza kupunguza government expenditures tukaenda kuboresha maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tuangalie zile ambazo hazina madhara ya moja kwa moja kwenye miradi ya wananchi vijijini na badala yake tushughulike na expenditures zingine ambazo tunaziweka kwenye on hold kwa muda mrefu. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Awali ya yote naomba nitoe salamu za pongezi sana kwa Serikali sikivu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya kwa ajili ya kukuza uchumi na kuboresha maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili ya salamu za shukrani zimfikie Mheshimiwa Luhaga Mpina, Mbunge, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, pamoja na timu yake yote Wizarani. Salamu hizi zinatoka kwa wananchi wa Hanga Ngadinda katika Halmashauri ya Wilaya ya Madaba. Wananchi hawa kwa muda mrefu wamehangaika sana kupata eneo la kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hekima kubwa na kwa uzalendo Mheshimiwa Waziri amekubali kuwapa hekta 1,800 ili kutatua tatizo la wananchi hawa. Tunamshukuru sana, sana, sana. Mheshimiwa Luhaga Mpina amekuwa mmoja katika Mawaziri ambao wapo tayari kuchukua maamuzi magumu yanayotatua matatizo ya wananchi. Tunaomba Serikali pia itambue mchango mkubwa wa Waziri huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba nijielekeze kwenye kuishauri Serikali katika mambo muhimu yanayohusu kukuza uchumi, hatutapata Tanzania ya viwanda kama hakuna uratibu wa pamoja wa sekta na Wizara zinazotegemeana. Hizi Wizara zinazotegemeana tunaziita Line Ministry. Ili upate Tanzania ya viwanda unahitaji uratibu wa pamoja wa Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Nishati na Madini, Wizara ya Viwanda na Biashara pia kwa karibu sana na Wizara ya Ardhi.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malighafi asilimia 65 inayohitajika viwandani au niseme viwanda kwa asilimia 65 vinategemea malighafi kutoka katika sekta hizi nilizozitaja ambazo ni sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi, madini lakini ardhi ndiyo Mama katika haya yote ambayo nimeyataja. Kama hakuna uratibu wa pamoja wa hizi Wizara hatutaipata Tanzania ya viwanda.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na eneo la kilimo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye hotuba yake ameondoa vikwazo vingi sana vya biashara, tunamshukuru na tunampongeza sana, hatua aliyoichukua itatatua tatizo la kufanya biashara nchini na ufanyaji biashara utakuwa rahisi zaidi, lakini Mheshimiwa Waziri wa Fedha amesahau sekta Mama ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania, sekta ya kilimo. Kwenye mchango wangu wakati nachangia Wizara ya Kilimo nilisema, hatutaweza kupata mapinduzi ya kilimo kama hatutawekeza kwenye usambazaji wa pembejeo na usambazaji wa pembejeo vijijini unakwazwa na gharama kubwa za kufungua maduka ya pembejeo na gharama hizo zinachangiwa na TFRA, TPRI, TOSC na TFDA.

Mheshimiwa Naibu Spika, tozo hizi Mheshimiwa Wazri Mkuu alizijibia humu ndani. Mheshimiwa Waziri wa Fedha naomba urejee kwenye majibu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu hizi tozo zinazokwaza uendelezaji wa sekta ya kilimo. Huwezi kupata mapinduzi ya kilimo kama hautaki kuwekeza kwenye usambazaji wa pembejeo. Sasa mtu wa kijijini anayetaka kufungua duka la kusambaza pembejeo na ninaposema pembejeo maana yake mbegu bora, mbolea na viuatilifu, kama hivyo havipo huwezi kupata mapunduzi ya kilimo. Kwa hiyo Mhehsimiwa Waziri wa Fedha naomba rejea kwenye majibu ya Waziri Mkuu kaondoe hizi tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Fedha ondoa tozo kwenye TFRA shilingi 100,000, ondoa tozo kwenye TPRI shilingi 320,000, ondoa tozo kwenye TOSC na TFDA ili mjasiriamali wa kijijini aweze kufikisha pembejeo kwa wakulima wadogo bila hivyo huwezi kupata mapinduzi ya kilimo na usipopata mapinduzi ya kilimo hakutakuwa na Tanzania ya viwanda. Hili ni muhimu sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na kama kutakuwa na fursa ya kushika shilingi Mheshimiwa Waziri wa Fedha, wote tunaoamini kwamba wakulima ndiyo mtaji mkubwa wa Watanzania na mtaji mkubwa wa CCM tutasimama na tutashika shilingi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema sekta hizi Mama zisipofanyakazi pamoja hatutapata mapinduzi ya viwanda. Ninaomba pia Waziri wa Fedha akubali kuziratibu hizi Wizara zote nilizozitaja. Ukisoma kwenye hotuba ya Waziri wa Kilimo ana vipaumbele vya mazao, atakuambia katika msimu huu kipaumbele changu ni mazao moja, mbili, tatu, nne huyo ni Waziri wa kilimo. Ukienda kwa Waziri wa Viwanda na Biashara ukisoma kwenye hotuba yake Waheshimiwa Wabunge mkasome mtaona baadhi ya mazao ambayo yamepewa kipaumbele na Wizara ya Viwanda na Biashara hayapo kwenye vipaumbele vya Wizara ya Kilimo sasa huyu anayeenda kuzalisha viwanda malighafi anazitoa wapi? Kwa hiyo, uone kwamba hapa ni kama hakuna coordination. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili upate mapinduzi ya viwanda unahitaji coordination. Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Nishati na Madini, Viwanda na Biashara na Wizara ya Ardhi mkubali sasa kukaa pamoja, kutengeneza mpango kazi wa pamoja, utaratibu wa joint planning, mfanye joint evaluation na monitoring ili tuweze kuipata Tanzania tunayoitaka.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya muda, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Jemedari Dkt. John Pombe Magufuli na wasaidizi wake akiwemo Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kufanya kazi iliyotukuka kwa Watanzania kwa miaka hii mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu jambo kubwa ambalo limejitokeza ni dhana ya uchumi jumuishi (inclusive economy). Mfumo huu wa uchumi jumuishi ni uchumi ambao unatoa fursa kwa Watanzania wote, kwa wananchi wote kuweza kunufaika nao. Dhana hii inatofautiana na dhana ya uchumi ambao sio jumuishi (extractive economy) ambayo inawanyima fursa watu walio wengi kuweza kushiriki kwenye uchumi au kunufaika na uchumi. Unawakumbatia mabeberu wachache na mabepari, hautoi fursa kwa watu wengi na watu wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu kwa miaka hii mitano imekuwa inatekeleza dhana ya uchumi jumuishi na imekuwa inafanya hivyo kwanza kwa kujenga mazingira na miundombinu wezeshi inayomfanya kila Mtanzania aweze kushiriki na kunufaika na uchumi wa Taifa lake. Imefanya hivyo kwa kujenga miundombinu ya reli, sasa programu kubwa ya ujenzi wa reli za kisasa imeanza na hii ya SGR inayoendelea sasa ni hatua ya kwanza na naamini tutaendelea kujenga reli. Pia programu kubwa ya umeme. leo Serikali imefikia vijiji 9,001 kutoka vijiji 2,118; ni achievement kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kutafsiri hii dhana ya uchumi shirikishi, Serikali imewekeza kwenye usafiri wa anga ili Watanzania waweze kujenga uchumi wao kwa kusafiri kwa haraka na kufanya mambo mengine ikiwemo uchumi wa utalii, lakini pia dhana hii tunaitafsiri kwenye namna ambavyo Watanzania wananufaika na ukuaji wa uchumi. Tunaona uchumi wetu unakua kwa asilimia 6.9. Kwenye maisha ya Mtanzania ananufaika nao vipi? Serikali imefanya kazi za kutukuka kwenye eneo hili. Leo tuna huduma za afya kwa kupitia vituo vya zahanati zaidi ya 1,198, Watanzania kwa maelfu wanapata huduma huko. Lakini tuna vituo vya afya, hospitali 69 mpya na hospitali za rufaa kumi, hiyo ni sehemu tu ya tafsiri ya ukuaji wa uchumi ambao umejengwa na Awamu hii ya Tano.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo nina ushauri wa mambo ya nyongeza kwa Serikali; kazi iliyofanyika ni kubwa sana, tumeona uchumi unakuwa na miundombinu inakuwa na mazingira wezeshi ya kiuchumi yanajengwa na Watanzania wananufaika na uchumi wao. Hata hivyo kuna mambo ambayo Serikali inapaswa kwenda kuyatafakari.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia takwimu za ukuaji wa uchumi ambao tumesema unakuwa kwa asilimia 9.9, sekta zilizochangia ukuaji huo zinatofautiana kwa umuhimu lakini Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo inaajiri asilimia 64 ya Watanzania ukuaji wake ni asilimia 3.6 wakati sekta zingine ambazo zimechangia kwenye ukuaji wa uchumi wa Taifa letu kama ujenzi unakua kwa asilimia 14.8, mchango wake kwenye ajira ni asilimia 2.42.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia uchukuzi, unakua kwa asilimia 8.8 lakini mchango wake kwenye ajira za Watanzania ni asilimia 2.94; ukiangalia huduma za usambazaji maji vijijini mchango wake kwenye ajira ni 0.05. Tafsiri yake ni nini; tafsiri yake eneo ambalo linawagusa Watanzania wengi ambao ni asilimia 64 mchango wake wa ukuaji ni mdogo sana ambao ni asilimia 3.6. Niiombe sana Serikali; dhana ya uchumi shirikishi ni kuwafikia hawa Watanzania walio wengi ambao sehemu kubwa ya maisha yao wanategemea kilimo. Nikiri, Serikali imefanya kazi kubwa kwenye kilimo, lakini kazi bado haijakwisha. Niiombe Serikali tunavyoendelea na mchakato huu wa bajeti ifikirie sasa kwenda kuwekeza zaidi kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, pili, Watanzania wengi, asilimia 60 mpaka 70 wanaishi vijijini. Dhana ya uchumi shirikishi au uchumi jumuishi ni kuwawezesha Watanzania hawa kuweza kushiriki kwenye uchumi. Watashiriki vipi kama barabara zao hazipitiki? Leo maeneo mengi ya vijijini bado yana changamoto na mafuriko ya mwaka huu yatufumbue macho tuone kwamba yapo maeneo ambayo tunahitaji kwenda kuwekeza nguvu zaidi.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wengi wapo maeneo ya vijijini. Kule Madaba kuna Vijiji vya Ifinga, kilometa 48 hazipitiki msimu mzima wa mvua, lakini huko ndiko kwenye Mbuga ya Selous na huko ndiko kwenye Watanzania ambao wanahitaji kushiriki kwenye uchumi. Niiombe Serikali yangu Tukufu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kuwekeza pia kwenye miundombinu ya barabara, miundombinu ya uchumi vijijini ili Watanzania walio wengi wanaoishi katika maeneo hayo waweze kunufaika zaidi na uchumi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, pia nimshukuru Mheshimiwa Rais na wananchi wa Madaba kwa kupata fursa ya kutumikia jimbo la Madaba kwa awamu ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja katika mambo makubwa ambayo yamejitokeza kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, ni hoja na haja ya kuwa na uwekezaji jumuishi katika kilimo. Hili Mheshimiwa Rais alilipa kipaumbele kwenye hotuba yake kwa sababu kubwa tatu.

Mheshimiwa Spika, sababu ya kwanza sekta hii imeajiri zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania, lakini sababu ya pili ni kwamba asilimia kumi au zaidi ya Watanzania ambao hawajishughulishi moja kwa moja na kilimo wamejiajiri kupitia sehemu ya mnyonyoro wa thamani wa shughuli za kilimo. Wapo waliojiajiri kwenye biashara ya mazao ya kilimo, wapo waliojiajiri kwenye usindikaji kwa maana ya agro-process, wapo ambao wamejiajiri kwenye kutoa huduma za kifedha yakiwemo mabenki, SACCOS, wapo waliojiajiri kwenye usambazaji wa pembejeo, lakini pia wapo wengi waliojiajiri kwenye huduma za ugani.

Mheshimiwa Spika, sababu ya tatu ni kwamba sekta hii ndiyo inayochangia asilimia mia moja ya chakula cha Watanzania wote. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais alitoa kipaumbele kikubwa sana katika kueleza namna gani sekta hii ipewe kipaumbele na ipewe msukumo katika safari hii ya miaka mitano sehemu ya pili ya kipindi chake cha miaka kumi.

Mheshimiwa Spika, leo naomba nitoe ushauri wa namna nzuri sasa ya kutekeleza maelekezo haya, ndoto na matamanio ya Mheshimiwa Rais kwenye sekta hii ya kilimo. Vitu ambavyo au jambo pekee ambalo linamfanya Mtanzania, mkulima aende shambani akawekeze kwenye kilimo, kivutio au incentive ya mtu kwenda kulima ni upatikanaji wa soko la uhakika na tija kwenye kilimo. Mambo makubwa yanayomfanya Mwanamadaba, Mwanasongwe na Mtanzania mwingine aache shughuli zingine akalime ni soko na tija kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alitoa kipaumbele miaka mitano iliyopita na kumekuwa na mafanikio, mipaka ilifunguliwa, masoko walau yalikuwa na unafuu. Hata hivyo, bado changamoto ni kubwa kwenye sekta hii upande wa tija kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, nina mambo mawili ya kushauri na kabla sijashauri nimpongeze Profesa Mkenda na Naibu Waziri Mheshimiwa Bashe wameanza vizuri sana katika kukabiliana na changamoto za sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ambalo napenda Serikali iendelee kuweka msisitizo ni kuwa na mkakati madhubuti wa masoko ya kilimo, bado hatujafaulu. Wakulima wa Madaba na maeneo mengine hata msimu huu wamepata shida ya soko la mahindi. Kwa hiyo ipo kazi kubwa ya kufanya. Namshauri Mheshimiwa Waziri aangalie sana mkakati endelevu wa kuimarisha vyama vya ushirika ili vitumike kama sehemu ya kupambana na changamoto ya soko lakini mkakati wa uwekezaji kwenye usindikaji wa mazao, sekta hii ni sekta mama ambayo itatutoa.

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili ambalo nitatumia muda mrefu kulifafanua ni hili la kuwekeza kwenye kupunguza gharama za kilimo. Jitihada zilizofanyika miaka hii mitano zimeonekana za kuhakikisha kwamba wakulima wanapata masoko ya mazao lakini hata pamoja na masoko kupatikana faida ambayo mkulima anaipata kutokana na shughuli zake bado ni ndogo kwa sababu gharama za uwekezaji kwenye kilimo ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa mambo mengi yanayochangia mambo matatu nataka niyaseme. Jambo la kwanza linalochangia gharama ya uzalishaji ni upatikanaji wa pembejeo kwa gharama nafuu. Jambo la pili ni gharama za usafirishaji wa mazao maeneo ya vijijini na jambo la tatu ni upotevu na uharibifu wa mazao baada ya mavuno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo mkulima yupo Madaba na maeneo mengine ya vijijini, huko ndiko alikojaa Watanzania, huko ndiko wanakokaa asilimia 80 ya Watanzania na wanajishughulisha na kilimo. Moja ya vikwazo ambavyo nimevisema ni upatikanaji wa pembejeo kwa gharama nafuu. Hili la upatikanaji wa pembejeo lina mawanda mapanda, lakini moja katika maeneo ambayo nataka nisaidie na kuishauri Serikali ni uwekezaji kwenye maduka madogo madogo ya kusambaza pembejeo vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pembejeo nyingi zinapatikana mijini na huko vijijini ambapo wakulima wapo hakuna maduka ya kusambaza pembejeo. Mkulima ili azalishe anasafiri kilometa nyingi kufuata pembejeo mijini. Suala hili nililisema katika Bunge lililopita. Sasa kinachokwaza upatikanaji wa maduka ya pembejeo vijijini ni gharama za uanzishaji wa maduka. Hapa ningeweza kwenda kwa details, lakini TPRI, TFRA na TOSCI peke yao ili upate kibali cha kuwekeza kwenye duka la usambazaji pembejeo kijijini lazima uwe na laki nane ambayo haihusishi kununua mali ghafi. Sasa hatuwezi kupata mapinduzi ya kilimo kama hatutaki kutoa hizi tozo. Hatuwezi kumsaidia mwananchi wa kijijini kupata pembejeo kwa gharama nafuu kama hatutaki kupunguza hizi tozo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili tutaenda nalo lakini naomba tulizingatie. Tuondoe hizi tozo ili tusaidie wajasiliamali wawekeze kwenye maduka madogo madogo ya pembejeo vijijini ili mkulima apunguziwe gharama za uzalishaji kilimo ili hata kama atakosa soko nzuri bado atauza kwa faida kwa sababu atakuwa amezalisha kwa gharama ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili ni gharama za usafirishaji wa mazao vijijini. Nashukuru Mheshimiwa mama Kilango amesema Watanzania wengi wamejaa vijijini, huko ndiko kwenye changamoto kubwa za miundombinu ya barabara na madaraja. Bajeti ya TARURA ni ndogo sana kuweza kukidhi mahitaji yaliyoko vijijini. Leo mkulima amelima mazao yake ili kusafirisha sehemu ambayo angesafirisha kwa shilingi laki moja anasafirisha kwa laki tano, hiyo inaongeza gharama za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa mama Kilango amesema ipo haya ya kuangalia uwezekano wa kuongeza bajeti TARURA ili barabara za vijijini zijengwe katika ubora, zipunguze gharama za uzalishaji kwa mkulima mdogo. Ndiyo maana nasema ni mkakati jumuishi wa sekta ya kilimo, sekta ya kilimo haiwezi kukua kama barabara za vijijini hazijaboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu nililotaka kuliongelea na kuishauri Serikali ni kwamba Serikali iangalie namna gani itapunguza upotevu na uharibifu wa mazao baada ya mavuno. Tafiti zinaonyesha asilimia 30 ya mazao ya mkulima yanaharibika baada ya mavuno. Sasa hii asilimia 30 kama ingeweza kufika sokoni ingempa faida huyu mkulima mdogo. Leo mkulima mdogo pamoja na gharama kubwa za uzalishaji inazotokana na kutopatikana pembejeo kwa wakati na karibu pamoja na gharama kubwa za usafirishaji bado…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, hoja yako ni ya msingi sana lakini muda hauko upande wako.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano. Mpango huu wa Tatu wa Miaka Mitano unajengeka toka kwenye Mpango wa Pili wa Miaka Mitano ambao tumeukamilisha utekelezaji wake mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja katika mambo makubwa ambayo yamebebwa na Mpango huu, ni dhana ya kujenga misingi ya uchumi wa viwanda. Na hapa nitaweka mkazo, kujenga msingi wa uchumi wa viwanda. Maana yake nini, tuliamua, kwenye ujenzi huu wa uchumi wa viwanda au ujenzi huu wa msingi wa uchumi wa viwanda uzingatie viwanda vyenye sifa kubwa mbili. Sifa ya kwanza, viwanda vinavyotumia malighali ya ndani. Lakini sifa ya pili, ni viwanda ambavyo vitatoa huduma au vitakuwa na impact kwa watu wengi, kwa maana ya critical mass. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunapoongea viwanda vinavyogusa au viwanda ambavyo vitatumia malighafi ya ndani, moja katika eneo muhimu sana ambalo lingetupa malighafi ambayo sio tu yanakwenda kutengeneza viwanda lakini nayo ni msingi wa viwanda ni chuma ya Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika huu ni karibu ni mwaka wa 20 au zaidi tunaongea kuhusu kwenda kuchimba chuma ya Liganga. Labda niseme mawili au matatu kuhusu hii Chuma ya Liganga. Kwanza inaambatana na uzalishaji wa umeme megawatts 600. Megawatts 600 ni robo ya umeme wote ambao tulikuwa nao mpaka mwaka 2015. Robo, yaani asilimia 25 sio mchango mdogo kwa uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo, ule mradi sio kitu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili, mradi wa Liganga na Mchuchuma unaenda kuzalisha iron owl chuma ngumu, tani milioni moja kwa mwaka. Sio jambo dogo, lakini sasa manufaa ya malighafi ya chuma ni makubwa sana kwa uchumi wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuma ya Liganga ingeweza kuzalisha viwanda vya nondo vya kutosha na vya kumwaga nchi hii, Chuma ya Liganga ingeweza kuzalisha viwanda vya mabati nchi hii, ingeweza kuzalisha viwanda vya baiskeli na vipuri vya magari vya kutosha kwa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, jaribu kufikiria ni viwanda vingapi na vya aina ngapi vingeweza kuzaliwa kutokana na uchimbaji wa chuma ya Liganga na Mchuchuma ukiachilia mbali suala zima la ajira kwa watanzania walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo nyakati pia tujifunze kwenye mataifa mengine Marekani, waliamua kuchelewesha ujenzi wa reli ili kujenga uwezo wa ndani wa kuchimba chuma yao ili wajenge reli yao kwa kutumia chuma yao. Maana yake ndio soko la kwanza la chuma yao ilikuwa ujenzi wa reli yao. Sisi nasi tuna fursa kubwa kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwenye eneo hili nimuombe sana Waziri wa Fedha, Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, arejee kwenye ajenda zetu tangu mwanzo huwezi kujenga uchumi wa viwanda Tanzania kama hutaki kwenda kuchimba chuma ya Liganga. Tutadanganyana, tutapiga kelele hapa, miaka itapita, nyakati zitabadilika na vizazi vijavyo vitatushangaa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, tulivyosema tunataka tujenge viwanda ambavyo vitatumia malighafi ya ndani na vina critical mass tulisema viwanda ambavyo vita- absolved bidhaa na mazao ya wakulima kwa asilimia kubwa. Mambo niliyotarajia niyaone kwenye Mpango wa mwaka 2015/2016 – 2020/2021 moja nilitaka nione viwanda vingi vya kusindika mazao ya kilimo na mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ametoa mifano ya viwanda lakini ukivipima kwa mizani, viwanda ambavyo vina critical mass effect ni vi chache sana ambavyo vinagusa mazao ya ngozi, vinagusa mazao ya kilimo. Mheshimiwa wa Wiziri wa Fedha ulikuwa kwenye Wizara ya Kilimo, unajua huwezi kukuza kilimo kama hutakuza viwanda vinavyosindika mazao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nina aamini, wakati huu upele umempata mkunaji na mkunaji ndio Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba ulikuwa kwenye sekta ya kilimo sasa upo kwenye Wizara ya Fedha peleka fedha kwenye kilimo, peleka fedha kwenye ku-facilitate kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kupata mapinduzi ya viwanda kama hutaki kuwekeza kwenye utafutaji wa masoko ndani na nje ya mipaka yetu ya Tanzania. Leo tunaongelea barabara za mipakani bado hazipitiki hazina lami, soko kubwa la Mazao ya mkoa wa Ruvuma tunategemea Msumbiji lakini tunatumia barabara ya vumbi. Hatuwezi kujenga uchumi kama hatutaki kutengeneza miundombinu ambayo itakuza biashara, itakuza viwanda. Na mimi naamini hii kengele ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo hoja tatu za haraka. Eneo la tatu, uwekezaji kwenye biashara unahitaji facilitation na hapa tuna mifano mingi sana leo, tunataka tuingie kwenye soko la Dunia lakini hatujaweka mechanism ya kutosha kuwawezesha wafanyabiashara wa Tanzania kuweza ku-meet vigezo kwa maana ya quality and quantity demands za soko la nje, hatutaweza! Hatutaweza kufika huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja zilizobaki nitazihifadhi lakini nilitaka niseme tunapotaka kubadilisha uchumi wa nchi yetu pia lazima tuwekeze kwenye diplomasia ya uchumi, lazima tuwe na mazuri na majirani zetu, lazima tuunganishe nguvu zetu za ndani na nje ili tulete mapinduzi ya uchumi kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia. Awali ya yote nampongeza sana Waziri Mheshimiwa Aweso kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye Wizara hii. Mheshimiwa Aweso ni mmoja katika Mawaziri ambao wanawafahamu wananchi wa Madaba na anafahamika na wananchi wa Madaba. Ametutembelea na kuangalia changamoto zetu katika Kijiji cha Mtyangimbole, lakini pia amekuja Mdaba Mjini Lituta, ameenda pia Kijiji cha Mtepa, Wino na pia amechangia fedha zake kuwezesha miradi ya maji ya wananchi. Ni mmoja katika Mawaziri wa kupigiwa mfano. Kwa niaba ya wananchi wa Madaba namshukuru sana sana Waziri Aweso kwa ushirikiano mzuri anaowapa wananchi wa Madaba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa kupitia Wizara ya Maji kwa kufanikisha miradi ya Madaba Mjini, tumefaulu kwa kiwango kizuri lakini bado hatujamaliza ule mradi kwa asilimia mia moja. Nimwombe Mheshimiwa Aweso kwamba eneo la Mtepa, Lituta na Kipingo maeneo ambayo tayari amekwishatembelea yamepata maji kwa kiwango, lakini kwa sehemu kubwa bado hatujamaliza usambazaji. Tunaomba Waziri aendelee kutupa support kwa kupitia timu yake ya mkoa na wilaya ambao kwa sasa wamefanya kazi nzuri sana, tunaomba aendelee kuwatia nguvu wafanikiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri yetu ya Madaba tunao mradi mmoja mkubwa sana wa vijiji nane na Mheshimiwa Waziri anavifahamu. Vijiji hivyo nane, ni Rutukira, Ndelenyuma, Bangamawe, Ngadinda, Ngumbiro, Mtyangimbole, Ruhimba na Likarangiro. Vijiji hivi havikuwa na maji kabisa, tulianza mchakato na Mheshimiwa Waziri kutafuta fedha bilioni sita kwa ajili ya ujenzi wa mradi mkubwa utakaotoa maji Mgombezi kupeleka kwenye vijiji hivi nane. Hata hivyo ilionekana hizi fedha ni nyingi na haziwezi kupatikana kwa mara moja. Ushauri wa Wizara na wataalam ulikuwa twende kwa vipande vipande.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru Serikali imeshatenga fedha milioni 350 kwa ajili ya Mradi wa Maji Rutukila na Ndelenyuma, lakini tayari imetenga fedha milioni 300 kwa Kijiji cha Mbangamawe kwa ajili ya kuanza kutekeleza mradi, lakini pia Kijiji cha Mahanje milioni 250. Jumla ya fedha iliyotengwa ni bilioni moja na milioni mia moja na tisa (Sh.1,109,000,000) kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa vijiji vinne; kati hivyo vijiji vitatu vinatoka katika vile vijiji nane nilivyokwishavitaja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapompongeza Waziri kwa kukubali kutenga fedha hii na Serikali kufanya hivyo, ninao ushauri wa kuhakikisha namna gani tunatekeleza miradi hii kikamilifu. Uzoefu unaonyesha mifumo ya utekelezaji ndio iliyoikwamisha Wizara hii kuwafikishia maji watanzania. Moja kati ya mambo ambayo napendekeza, eneo la kwanza utamaduni umekuwa kuunda kamati za utekelezaji wa miradi hii baada ya miradi kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kamati ziundwe kabla ya mradi haujaanza, kamati zishiriki kwenye utekelezaji wa mradi ili wanapokabidhiwa mradi wajue changamoto za mradi. RUWASA watekeleze miradi yote kwa kushirikiana na Kamati za Maji tangu day one hii itasaidia sustainability.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na ushauri wa maeneo mengine matatu, lakini nimesikia kengele imepiga, nataka niongeze umuhimu wa kuhakikisha kwamba mifumo ya kuingiza maji kwenye nyumba, pale Madaba tuna shida, tunawataka wanaotaka kuingiza maji kwenye nyumba waje wanunue mabomba RUWASA.

Mheshimiwa Naibu Spika, inatosha kutoa viwango vya ubora vya mabomba yanayotakiwa, mteja akanunue mwenyewe vifaa vyote, RUWASA wakague wamsaidie mteja. Mfumo tulioweka sasa Mheshimiwa Waziri wananchi wanaamini kwamba ni mfumo unaowezesha watu kupiga fedha, hatutaki kuwapa wananchi fursa ya kutafsiri vibaya nia njema ya Serikali ya kuwawezesha, tuwaachie wananchi wakanunue vifaa. RUWASA wakague vifaa hivi vimefikia viwango viwekwe, sio wananchi wanunue kupitia RUWASA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa RUWASA kununua vifaa vya miradi kwa kutumia mfumo ambao ni centralized unachelewesha sana utekelezaji wa miradi maeneo ya miradi, waandae utaratibu mpya utakaowawezesha wilaya, halmashauri au RUWASA katika ngazi ya wilaya na mkoa kununua vifaa wenyewe moja kwa moja kwa sababu hiyo centralized system ni nzuri lakini inachukua miezi sita mpaka saba kupata vifaa tunavyotaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wanapata maji, Mheshimiwa Aweso amekuwa makini na Naibu wake Waziri, hawajatukatisha tamaa, nasi tunawatia moyo wanaweza, tuhakikishe kwamba Watanzania wanapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba hii muhimu inayowahusu asilimia 80 ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameweka vipaumbele vya majukumu ya Wizara katika bajeti ya mwaka huu na kipaumbele namba tano (5) ni soko la mazao ya kilimo. Ningepata fursa, ningeweza kurekebisha hotuba yake na kusema kipaumbele namba moja (1) kiwe soko la mazao ya mkulima. Nasema hivi kwa nini? Kwa sababu mwarobaini wa Sekta ya Kilimo ni soko. Msingi wa kilimo ni soko. Katika mnyororo wa kilimo kuna shughuli mbalimbali ikiwemo uzalishaji, usafirishaji, usindikaji, masoko, lakini soko ndiyo dereva anayeendesha Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale ambapo mkulima ana uhakika wa soko, pale ambapo mkulima atakuwa anauza zao lake kwa faida, hatahitaji kukusubiri wewe umletee Afisa Ugani, atamtafuta yeye mwenyewe, atamwajiri yeye mwenyewe kwa sababu kuna faida kwenye kilimo. Ili kilimo kiwe na faida lazima tuwekeze kwenye masoko. Ukishawekeza kwenye soko una-create incentive ya mkulima kuzalisha, akiona inamlipa atatafuta Maafisa Ugani, huko ndiko tupeleke fedha.

Mheshimiwa Spika, ili kilimo kiwe na faida lazima tuwekeze kwenye masoko. Ukishawekeza kwenye soko una- create incentive ya mkulima kuzalisha akiona inamlipa atatafuta maafisa ugani, huko ndiko tupeleke fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakupa mfano, kwenye Bunge lako kwa miaka yangu yote sita sijawahi kumuona Mbunge anayehamasisha vijana wakanunue bodaboda, lakini vijana wanaenda kununua bodaboda kwa sababu, bodaboda zinawalipa, hiyo ndiyo essence ya kuwekeza kwenye kitu kinacholipa. Hatujafanya promotion ya bodaboda nchi hii, lakini Watanzania vijana wetu wanawekeza kwenye bodaboda na sio kwenye kilimo cha mahindi; hawawekezi kwenye maharage kwa sababu, maharage hayalipi kwa sababu hatujawekeza kwenye soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri abadilishe vipaumbele vyake kipaumbele namba moja kufanya mapinduzi ya kilimo nenda kawekee kwenye soko. Soko ndio lita-create demand ya maafisa ugani, lita- create demand ya processing, n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya kwenye soko ni nini? Moja changamoto Mheshimiwa Waziri vitu ambavyo anatakiwa kuvijua ni vitatu; changamoto ya kwanza kwenye soko ni upatikanaji wa masoko yenyewe ya mazao. Mwaka jana wakulima wa Mkoa wa Ruvuma wameibiwa sana fedha zao, wamedhulumiwa sana mahindi kwa sababu, hatuna soko la uhakika la mazao ya mahindi. Wameenda kuuza kwa msanii mmoja pale Mkako mamilioni ya fedha yamepotea. Mheshimiwa Waziri ajue changamoto ya kwanza ni upatikanaji wa masoko ya mazao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya pili kuhusu masoko ya mazao ya kilimo ni miundombinu ya masoko ya mazao ya kilimo. Na tunapoongea miundombinu ni dhana pana na sitaweza kuifafanua kwa kina, lakini Profesa Mkenda na Ndugu yangu Mheshimiwa Bashe ni wabobezi kwenye eneo hili. Tukisema miundombinu ya kilimo tuangalie maghala na maeneo ya kuhifadhia mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, soko lina specifications zake. Soko la mahindi ya Kenya wanataka mahindi ambayo hayana sumu kuvu, ili uweze kukidhi hitaji hilo lazima uwe na uhifadhi ambao utasaidia mahindi yako yanapokwenda Kenya yawe hayana sumu kuvu. Hiyo ndio miundombinu ya masoko, tuwekeze kwenye maghala na vifaa vya kuhifadhi ubora wa mazao yetu ili yawe shindani kwenye masoko tunayoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili kuhusu miundombinu ni miundombinu ya barabara. Hii imefafanuliwa na Mwenyekiti wa Bajeti amesema. Kwa maslahi ya muda nitaruka eneo moja muhimu sana la miundombinu ya masoko naomba niende kwenye mfumo wa masoko.

Mheshimiwa Spika, mifumo ambayo tunaitumia kuuza mazao yetu ipo mingi, lakini hapa nitaitaja mitatu; tuna mfumo wa kilimo mkataba, tuna mfumo wa stakabadhi za ghala (warehouse receipt system), tuna mfumo wa TMX ambao nadhani tutakuwa tumeuchukua Ethiopia. Hii mifumo mitatu ningepeta nafasi ningeifafanua kwa kina faida na hasara zake. Lakini namuomba Mheshimiwa Waziri, Profesa Mkenda, naomba nenda kafanye assignment kuhusu kilimo mkataba, faida zake ni zipi. Moja ya faida muhimu ya kilimo cha mkataba kinakusaidia ku-meet demand za soko in terms of quality na quantity. Lakini pia kinakusaidia kupata ku-raise capital ya kuzalisha. Wakulima wengi hawana mitaji na hatuna namna ya kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mfumo wa soko la stakabadhi ghalani hautekelezwi kwa mujibu wa kanuni na sheria zilizowekwa kuhusu soko la stakabadhi ghalani. Stakabadhi ghalani ya Tanzania imekuwa soko la kukusanyia mazao, hakuna stakabadhi ya ghala pale. Mkulima hapati pembejeo, mkulima hapati mbegu bora, hapati mbolea, hapati mtaji wa kwenda kulima, tunaita stakabadhi za ghala sio stakabadhi ya ghala hiyo, hiyo ni aggregation center, hiyoni collection center ya mazao sio stakabadhi ya ghala kwa sababu, ai-add value ya kutosha kwa mkulima. Mheshimiwa Waziri naomba ukafanyie assignment kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini tatu kafanyie assignment kwenye suala la TMX. Je, tunatumia modal gani ya TMX? Je, TMX ni complimentary ya warehouse receipt system au ni kitu kinachosimama peke yake? Unawezaje ku-implement TMX katika mazingira yetu kama huna maghala yenye ubora? Kama huna mifumo ya teknolojia inayoweza kukusaidia kuweza kuingia kwenye masoko shidani?

Mheshimiwa Spika, muda ni mchache sana, agenda hii ni pana. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Waheshimiwa Wabunge kukushukuru kwa kupata fursa ya kuzungumza, lakini kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Wizara hii kwa kazi kubwa na kwa ubunifu ambao wanao ili kuendeleza sekta ya uhifadhi na utalii nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee namshukuru Mheshimiwa Waziri baada ya kumweleza changamoto za wananchi wangu wa Jimbo la Madaba alikwenda mwenyewe, kwenda kuwasilikiza na kuanza mchakato wa kumaliza changamoto zao. Namshukuru sana Waziri na naomba aendelee na moyo huu huu. Nimemwona anakwenda Tunduru, nimeona anakwenda sehemu mbalimbali ndani ya nchi yetu kwenda kuwasikiliza Watanzania na kuona namna gani tunamaliza changamoto zao na naamini approach aliyonayo itatufikisha salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii ina changamoto kubwa sana, tumeipa mzigo mkubwa sana. Nchi hii inawategemea wakulima, inawategemea wafugaji, inawategemea watalii na inawategemea wahifadhi. Sekta hizi zote zinategemeana na Watanzania wanaongezeka kwa idadi. Changamoto ya Mheshimiwa Waziri ni namna gani tunaweza ku-accommodate tuka-strike balance miongoni mwa wafugaji, wakulima na hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu Mheshimiwa Waziri azingatie ushauri uliotolewa na baadhi ya Wabunge hapa wa kurejea upya michoro ya nchi hii ili kuweka bayana maeneo ya mifugo, maeneo ya kilimo na maeneo ya hifadhi ili kuhakikisha kwamba kila kitu kinapewa kipaumbele na Watanzania wanaishi kwa utulivu na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri pia aendelee kuangalia mgogoro wa wananchi wa Madaba kwa eneo la Slow ambalo tayari ameanza kulifanyia kazi. Wananchi hawa pamoja na kazi nzuri aliyoifanya Waziri, bado hawaamini kwamba lile eneo ni mali ya maliasili, wanaamini kwamba wameporwa. Naomba jukumu la maliasili siyo kushambulia wale wananchi, jukumu la maliasili ni kukaa nao chini na kuelekezana kwenye michoro, ni wapi inaonyesha kwamba ni mali ya maliasili na wapi ni mali ya vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya maeneo kama alivyosema Mheshimiwa Ng’wasi, yanatumia michoro ya zamani sana na tayari haya maeneo yameshatangazwa kuwa vijiji, Kijiji cha Nderenyuma kimetangazwa kwenye ziara ya mwisho ya Mheshimiwa Rais Marehemu Dkt. John Pombe Magufuli ameitanganza Nderenyuma kuwa Kijiji. Mbangamawe ni Kijiji cha muda mrefu, maeneo haya yote sasa maliasili wanasema kwamba ni kivuko cha wanyama kwa hiyo wananchi wasilime mazao ya chakula kama mahindi. Ni ushauri mzuri, lakini ukiwa participatory utatusaidia kumaliza mgogoro huu. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Neema Mgaya.

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa kaka yangu Mheshimiwa Joseph Mhagama kwamba tatizo hili la migogoro hii kati ya mipaka ya mapori ya akiba na hifadhi na vijiji vingi ndani ya Tanzania imekuwa tatizo kubwa sana na Wabunge wengi wanalalamikia tatizo hili. Ifikie mahali sasa Mheshimiwa Waziri waweze kutatua migogoro hii, wakae waende kwa pamoja na Waziri wa Ardhi ili mkienda kumaliza tatizo mnamaliza moja kwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano kule Wanging’ombe, alikuja Naibu Waziri wa Ardhi mwaka 2018, lakini mpaka leo lile tatizo halijamalizika, hebu wakae kwa pamoja na Wizara ya Ardhi muweze kumaliza matatizo haya…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Neema ahsante kwa mchango wako. (Kicheko)

Mheshimiwa Joseph Mhagama.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea kwanza taarifa ya dada yangu Neema Mgaya kwa sababu ya muda…

NAIBU SPIKA: Naambiwa na kengele ilikuwa imeshagonga hapa mbele.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri basi tuendelee kushirikiana na wananchi wa Madaba kumaliza changamoto zao kwa njia ya kushauriana. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha hoja. Kwanza kabisa niwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliopata nafasi ya kuchangia hoja hii jumla ya Wabunge sita walichangia hoja hii na niwatambue kwa majina Mheshimiwa Olelekaita Edward, Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mheshimiwa Salim Shafii, Mheshimiwa Joseph Tadayo na Mheshimiwa Asha Abdulla Juma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru Serikali nimepata fursa ya kufafanua hoja mbalimbali lakini pia imepokea maoni na ushauri wa kamati na ipo tayari kwenda kutekeleza na niwatambue Mheshimiwa Dkt. Selemani Jafo Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mheshimiwa George Simbachawene Waziri wa Katiba na Sheria, Mheshimiwa Balozi Daktari. Pindi Chana Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu na Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu kwa kufafanua baadhi ya hoja na kwa kukubali kuchukua hoja za Kamati ya Katiba na Sheria kwenda kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaielekeza au sijaiomba Serikali kuhusu hizi hoja za kamati katika ujumla wake, kuna mambo kadhaa ambayo ni vizuri kamati ikaweka msisitizo kwa kuzingatia ushauri wa wajumbe wa kamati lakini Wabunge walioweza kuchangia kwenye Bunge lako na hoja ambazo zimetolewa na Mawaziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kuna suala la uwezeshaji vijana, Mheshimiwa Waziri Profesa Joyce Ndalichako ameeleza vizuri kwenye eneo hili lakini ni vizuri tukaiomba Serikali izingatie na kutekeleza mpango kazi mpango mkakati ambao unao wa miaka mitano ambapo Serikali imekubali kutenga bilioni 550 ambapo kila mwaka itatoa bilioni 102 kwa ajili ya vijana 681,000 kuwawezesha katika sekta ya ajira. Tunadhani hili ni jambo muhimu sana Serikali ikalizingatia na hili litakuwa limeboresha sana sana huduma kwa vijana kwa sababu kabla yake tulikuwa tunawahudumia vijana 20,000 tu kwa mwaka lakini sasa tutaweza kuwafikia vijana 136,000 kwa mwaka ni mapinduzi makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kwa kibali chako eneo lingine ambalo limejadiliwa sana na Wabunge humu ndani ni eneo hili la OSHA. Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani amelisema, Mheshimiwa Tadayo lakini Mheshimiwa Asha Abdullah.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi hii ya OSHA, kwa ridhaa yako niiombe Serikali iichukulie kama miongoni mwa taasisi za mfano, ikibidi taasisi nyingine za Serikali zikajifunze kwenye taasisi hii. OSHA imeweza kuitambulisha Tanzania SADC na sasa ina dawati, kwa sababu inafanya kazi vizuri, lakini pia wana matumizi bora ya fedha wakati wa ujenzi wa jengo lao hapa Dodoma, imefanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo haya tumeiomba OSHA ijaribu kuji-align na blue print ili kuona namna gani inaweza kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara nchini. Tulitaka tutambue mchango mkubwa sana wa Mtendaji Mkuu wa taasisi hii. Nirekebishe hoja ya mjumbe wangu mmoja, alisema kwamba Mtendaji Mkuu hajathibitishwa; Mtendaji Mkuu amethibitishwa na anafanya kazi vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu lilikuwa ni kuhusu Kiwanda cha Viatu na Bidhaa za Ngozi (Kilimanjaro International Leather Industry Company Limited) na hapa pia kumekuwa na mchango wa Mheshimiwa Waziri. Sisi tunaamini kiwanda hiki, kwanza, kina fedha nyingi sana za wananchi kwa kupitia Mfuko wa PSSSF asilimia 86 ziko hapo, lakini kina tija kubwa sana kwa Watanzania wote wanaozunguka Mikoa ya Kilimanjaro, hasa wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo kiwanda hiki kitafanya vizuri kitatoa ajira kubwa sana kwa Watanzania. Zaidi ya Watanzania 3,000 wanategemea kupata ajira ya moja kwa moja na Watanzania 7,000 watapata ajira zisizo za moja kwa moja. Haya ni mapinduzi makubwa sana na ni mchango mkubwa sana kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi letu kama Kamati, waangalie teknolojia tunayotumia kutengeneza viatu hivi ili tuweze kupata teknolojia bora na shindani zaidi katika masoko ya ndani na ya nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la nne, ukipenda, ni mfumo wa utoaji haki nchini. Miongoni mwa maeneo ambayo tungependa tu-draw attention ya Wabunge ni namna ambavyo Serikali ya awamu ya sita imekusudia kwa dhati kabisa kusimika miguu Dodoma kama Makao Makuu. Ujenzi wa Jengo la Mahakama Kuu ambalo sisi kama Kamati tumetembelea leo ambalo lina three courts katika campus moja, maana yake kuna High Court, Supreme Court na Court of Appeal, ni kielelezo kwamba sasa mihimili yote mitatu ipo Dodoma, Serikali imesimika miguu Dodoma. Hilo tulidhani ni muhimu kulisema. Hili sasa linajibu hoja za wachangiaji walioonesha kwamba tuna changamoto kidogo kuhusu mfumo wa utoaji haki nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa jengo hili na upatikanaji wa watumishi kwenye eneo hili utaongeza kasi ya utekelezaji wa jukumu hili. Niiombe Wizara sasa, tuna upungufu wa watendaji, Wizara ilifanyie kazi hili. Vile vile kuna eneo muhimu la kukamilisha Sera ya Taifa ya Mashtaka, ilitakiwa iwe imekamilika by December, 2021, lakini mpaka sasa bado, pamoja na uharakishaji wa kanuni baada ya sheria kutungwa. Tunaomba Mheshimiwa Waziri ayachukue haya na ayafanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, kwanza niiombe Serikali iyafanyie kazi maoni na mapendekezo yote ya Kamati ya Katiba na Sheria kama yalivyowasilishwa mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja sasa kwamba Bunge lako lipokee Taarifa ya Kamati na likubali maoni na mapendekezo yote ya Kamati kama yalivyowasilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa unyeknyekevu kabisa na kwa niaba ya Kamati ya Katiba na Sheria tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote na Mawaziri walioweza kuchangia hoja hizi ambazo tumezileta mbele yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya Waheshimiwa Wabunge kumi na Mawaziri watano wamepata fursa ya kuchangia moja kwa moja kwa njia ya kuzungumza kwenye maeneo muhimu ambayo Kamati iliyaleta mbele ya kiti chako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maslahi ya muda nisingependa kuwatamka hapa, lakini tulikuwa na mambo kadhaa ambayo yamewekewa mkazo kwa Waheshimiwa Wabunge na nisingepende niende kuyaeleza yote, lakini niweke mkazo katika maeneo machache ambayo yameelezwa; moja, ni Mfuko wa Maendeleo ya Vijana umepata ufafanuzi wa kutosha sana kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge, lakini pia kwa Mheshimiwa Waziri Ndalichako mwenye dhamana katika eneo hilo tunatambua na tunaelewa mabadiliko ya taarifa kwa maana ya kwamba utekelezaji umefanyika baada ya sisi kupita kukagua. Kwa hiyo, tunashukuru kwamba mapendekezo ya Kamati yamefanyiwa kazi kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya lugha ya uandishi; imepewa ufafanuzi mzuri na tunashukuru kwa wadau kuliwekea msisitizo Idara ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali, lakini eneo la nne ni kazi na ajira.

Mheshimiwa Mwneyekiti, hili jambo limepata ufafanuzi mzuri kutoka kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri mwenye dhamana katika eneo hili, lakini pia wadau upande wa Serikali Mawaziri mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja kubwa ya Kamati na hoja kubwa ya Wabunge tunapotoa ajira za Serikali, ajira ambazo tunaenda kulipa kwa kutumia fedha ya umma tusimlinganishe mtoto aliyemeliza Madaba Day Secondary School na mtoto aliyemaliza Feza Boys na wote tukawashindanisha kwa viwango vinavyofanana na baadae tukajikuta kwamba ajira zote zinaelemea kwa watu wa aina fulani, watu wa aina moja, hiyo ndio hoja ya kamati na ndio hoja ya Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotoa ajira tufanye allocation kadri ya mikoa, tufanye allocation kadri ya wilaya. Tuna ajira 200; je, mkoa wa Ruvuma ziende ajira ngapi? Mkoa wa Morogoro ziende ajira ngapi ili watoto wa mkoa wa Ruvuma wapimwe kwa viwango vya mkoa wa Ruvuma, la sivyo tutakuja kujenga taifa lenye changamoto kubwa sana na hiyo ndio hoja ya Kamati na hiyo ndio hoja ya Wabunge na nakuomba ikikupendeza Waheshimiwa Wabunge waipitishe hoja hii kama ambavyo imewasilishwa na Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na hoja ya Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ya Uendeshaji wa Mashauri ya Jinai; Waheshimiwa Mawaziri wamefafanua pia na Waheshimiwa Wabunge wamesema, lakini hoja kubwa ya Kamati ni kuitaka Ofisi hii iheshimu maamuzi ya Mahakama hasa pale ambapo mahakama inatoa maamuzi juu ya watuhumiwa warudishiwe mali zao. Ofisi hii ihakikishe hayo yanafanyika na hiyo ndio hoja ya Kamati na ninaomba Bunge lako liipitishe kama ilivyopendekezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine zimepewa msisitizo mzuri ikiwemo hoja ambayo aliifafanua vizuri sana Mheshimiwa Khadija Taya inayohusu watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naomba sasa Bunge lako likubali kupitisha taarifa pamoja na maazimio yote ya Kamati ya Katiba na Sheria kama yalivyowasilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Ofisi ya Rais TAMISEMI muda huu wa asubuhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya uchumi jumuishi kwa maana ya inclusive economy ambapo kila Mtanzania atanufaika na ukuaji wa uchumi wa Taifa letu ni pale ambapo kila Mtanzania atakuwa amefikiwa na huduma muhimu na za lazima kama vile maji, umeme, barabara, afya na elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu hii ya Sita kwa sehemu kubwa imefaulu sana kwenye maeneo makubwa mawili au matatu. Kwa sehemu kubwa tumefaulu suala la umeme vijijini lakini changamoto bado zipo, linalohusiana na sehemu hii ya TAMISEMI tumefaulu sana kwenye eneo la elimu na afya hasa kwenye shule zetu za msingi na sekondari kwa bajeti kubwa ambazo zimetengwa kwenda kuboresha maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upande wa afya kwa kiwango kikubwa, fedha zimekuwa zinakwenda kwenye zahanati, fedha zimekuwa zinakwenda kwenye vituo vya afya na Hospitali za Wilaya na Hospitali za Rufaa tumeendelea kuzijenga. Kwenye eneo hili naomba niipongeze sana Serikali ya CCM chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie fursa hii kumpongeza sana Waziri Mheshimiwa Innocent Bashungwa pamoja na Manaibu Waziri wake wote wanafanya kazi nzuri sana. Nitumie pia fursa hii kumpongeza Katibu Mkuu Profesa Shemdoe haya ni majembe kwelikweli na wamefanya kazi nzuri katika maeneo hayo niliyoyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na nia nzuri na kubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita, pamoja na jitiahada kubwa ambazo Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuzifanya bado tuna changamoto kubwa kwenye barabara za vijijini. Nimesema ili Watanzania wanufaike na dhana ya inclusive economy ni lazima barabara za vijijini ziboreshwe na zijengwe kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ambayo imekuwa inatolewa bado haitoshi, Madaba Halmashauri yetu kwa miaka mitano mfululizo imekuwa ikipokea asilimia tano tu ya mahitaji yake yote ya barabara za vijijini. Madhara yake tumeendelea kuwa na barabara mbovu kwa muda mrefu. Hata hivyo, nitambue kazi kubwa ambayo Serikali imeifanya kwenye bajeti iliyopita ambapo alitoa zaidi ya Shilingi Bilioni Moja na Milioni Mia Tano ambayo kwa mahitaji ya Madaba ni asilimia 15 ya mahitaji ya barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweza kupiga hatua kwenye eneo hilo, nampongeza sana CEO wa TARURA na timu yake nzima na Serikali katika ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu Serikali itambue kwamba pamoja na kutoa fedha kiwango hicho, kwa Madaba yetu sisi hiyo ni asilimia 15 tu ya mahitaji halisi ya barabara Halmashauri ya Wilaya ya Madaba. Ndani ya Mji wa Madaba tuna kilomita 66 zimeanza kufunguliwa kwa maeneo ya Lituta na Madaba Mjini na bado hatujakidhi mahitaji ya Watanzania wanaoishi Madaba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Halmashauri ya Madaba tuna zaidi ya kilomita 642 ambazo zinahitajika kujengwa na kuboreshwa. Tuna madaraja yanayokwenda maeneo muhimu ya uzalishaji, ikiwemo Yerusalemu, Kwangoko, maeneo mengine ya Mtengimbole, Litepatile na maeneo yote ya Madaba tunayo changamoto kubwa ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri azingatie kwanza kuhakikisha kwamba bajeti iliyokusudiwa itolewe lakini fedha zaidi za ujenzi wa barabara vijijini ziongezwe, bila hivyo tutakuwa hatujakidhi matakwa ya kujenga uchumi inclusive ambao utawanufaisha Watanzania wengi hasa walioko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Madaba ni Halmashauri changa, mapato yake kwa asilimia kubwa yanawategemea wakulima wadogo wadogo na kwa sehemu nyingine tunategemea kilimo cha miti, ukiachana na hizo hatuna vyanzo vingine. Tunaomba Serikali itusaidie tujenge stendi ya Madaba ambayo itachangia asilimia 20 ya mapato ya Halmashauri ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia maslahi ya muda, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria. Mchango wangu utajikita kwenye Fungu Na. 35 la Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kwa maana ya DPP.

Mheshimiwa Spika, Kamati imeeleza nini imebaini kwenye Ofisi hii. Moja katika mambo makubwa ambayo imebaini ni kwamba Ofisi ya DPP ni Ofisi muhimu sana katika masuala ya utoaji haki, lakini bajeti ambayo imetengwa kwa ajili ya ofisi hii ni ndogo sana katika kukidhi mahitaji ya upatikanaji haki kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili hoja yangu ieleweke, naomba Watanzania wafungamanishe Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na dhana au Dira ya Tanzania ya kujenga uchumi kwa kupitia viwanda na biashara. Utakubaliana nami kwamba moja ya vivutio vikubwa vya uwekezaji na biashara nchini ni utawala wa sheria. Kama hakuna utawala wa sheria, hatutaweza kuvutia uwekezaji wa aina yoyote nchini.

Mheshimiwa Spika, wataalam wanasema, hatuwekezi biashara pale ambapo pana utawala wa viongozi, bali pale ambapo pana utawala wa sheria. Hapa ni mkazo juu ya utawala wa sheria dhidi ya utawala wa viongozi. Tanzania tumepiga hatua kubwa sana kwenye eneo hilo. Awamu hadi Awamu Tanzania imefanya transformation kubwa kutoka kwenye utawala wa viongozi kwenda kwenye utawala wa sheria. Hilo limejidhihirisha sana katika utawala wa Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Awamu hii ya Sita, tumeona namna Mheshimiwa Rais ameendelea kuweka mkazo wa ku-transform mfumo wetu wa utawala ili tuwe na utawala wa sheria ambao utatoa haki kwa Watanzania wengi, lakini pia itafungua fursa za kukua kibiashara. Miongoni mwa mambo ambayo tumefanikiwa sana katika kipindi hiki kifupi; moja, ni zaidi ya Watanzania milioni moja na nusu wamepata huduma ya ushauri wa sheria katika Wiki ya Sheria. Haya ni mafanikio makubwa. Lingine ni uteuzi wa Majaji. Ili kutoa huduma, ni Majaji katika Mahakama ya Rufani tisa na kufanya jumla ya Majaji wote katika Mahakama ya Rufani kufikia 21. Ni hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kumekuwa na uteuzi wa Majaji katika Mahakama Kuu Majaji 21 wameteuliwa na hivyo Majaji katika Mahakama Kuu kufikia 82. Hii ni hatua kubwa sana katika utoaji wa haki nchini. Sasa tuna Mahakimu 245, hayo ni mafanikio makubwa sana katika Awamu hii. Siyo hayo tu, unaona kwamba Mahakama imepanua wigo wa utoaji haki na imewapeleka Mawakili sasa waweze kutoa huduma kwenye Mahakama za Mwanzo ili kuwafikia Watanzania walio wengi ambao wanategemea sana Mahakama hizi za Mwanzo ili kupata huduma ya upatikanaji wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matumizi ya lugha ya Kiswahili kwenye Mahakama zetu ni hatua kubwa sana ambayo ni lazima tuiweke kwenye kumbukumbu za Taifa letu katika Awamu hizi zinazofuatana. Tumeona kuna mafanikio makubwa kwenye ujenzi wa majengo ya Mahakama, lakini pia Ofisi ya DPP imezidi kupanua huduma na sasa ina ofisi karibu katika Mikoa 26 za Kimahakama, lakini Wilaya 14. Hayo yote ni mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, nilitamani kabla sijatoa ushauri na mapendekezo yangu niwapongeze sana, kwanza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan; Waziri wetu, Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro, Naibu Waziri, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na timu nzima ya Wizara hii kwa kazi kubwa ambazo wamezifanya na mafanikio ni makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio haya makubwa ambayo nimeyaeleza bado tuna changamoto kubwa sana ya kuwafikia Watanzania walio wengi huko chini kwenye Mahakama za Mwanzo, ikiwemo Madaba, maeneo yote ya Songea Vijijini, hatuna huduma za uhakika zitakazompunguzia Mtanzania gharama ya kwenda kutafuta haki. Leo Ofisi ya DPP ina ofisi katika wilaya 14 tu, maana yake nini?

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba, katika wilaya nyingine za Tanzania zinazobaki mashitaka mengi yanaendeshwa na watu ambao hawana sifa ya kuendesha mashitaka. Askari Polisi ndio wanaokamata, Askari Polisi ndio wanaopeleleza, lakini ndio wanaoshitaki, haki ya Mtanzania itapatikana vipi kama utaratibu huu utaendelea hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, rai yangu ni kuiomba Serikali iiongezee fedha Ofisi ya DPP ili iweze kufika katika maeneo yote ya Tanzania, ili iweze kuwafikia Watanzania wanyonge ambao uchumi wao unategemea kulinda haki zao za ardhi na maeneo ya biashara. Watu wananyimwa haki za kufanya biashara katika maeneo mbalimbali, lakini hawana namna ya kutafuta haki hizo kwa sababu wanaotakiwa kulisimamia hilo hawana uwezo wa kufika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, ninasema haya kwa Ushahidi. Mpaka mwezi Februari, 2022 kesi za jinai zilizosimamiwa na Ofisi ya DPP ni 42,138 katika hizo ni asilimia 28 tu ya kesi zote zimepatiwa ufumbuzi, hizo nyingine zote zimebaki. Tunawasaidiaje Watanzania kumaliza changamoto hizo kama Serikali haipo tayari kuongeza fedha kwenye Ofisi ya DPP?(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, lakini naiomba Serikali iiangalie ofisi hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami ninaomba niungane na Waheshimiwa Wabunge waliowengi kwanza kabisa kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Daktari Rais Samia Suluhu Hassan kwa uzalendo wake mkubwa kwa Watanzania katika ujumla wake lakini mahususi kwa Watanzania wananchi wa Madaba.

Mheshimiwa Spika, Madaba katika kipindi hiki kifupi cha utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2022/2023 ambayo iyotakamilika Juni tayari Madaba tumeshapokea zaidi ya bilioni kumi na moja na milioni mia sita kwa ajili ya shughuli za maendeleo ikiwemo shilingi bilioni tatu na milioni mia tatu kwa ajili miradi ya maendeleo ya kawaida na mengineyo, TARURA zaidi ya bilioni mbili, miundombinu ya shule zaidi ya milioni mia sita na kumi na miradi mingine ya maji ambayo inafika karibu bilioni sita.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Madaba wamenituma nitoe shukrani za pekee sana kwa Mheshimiwa Rais, wanatambua sana kazi hizi zinazofanyika na Madaba inaendelea kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Angellah Kairuki Waziri wa TAMISEMI. Hapa mbele yangu nina taarifa mbalimbali zinazotoka Ofisi ya TAMISEMI kwa Mheshimiwa Waziri akitufahamisha Waheshimiwa Wabunge kuhusu miradi mbalimbali na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa maeneo yetu. Utaratibu huu ni mzuri sana unatusaidia sana kwenye ufatiliaji. Sisi ndiyo Wabunge tunaosimama hapa kuomba fedha kwa niaba ya wananchi wetu tunapopata taarifa kwa utaratibu huu mzuri ni lazima tupongeze tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Madaba tumefanikiwa mengi lakini bado tuna changamoto nyingi sana. Nitazisema mbili kwa leo lakini nafasi nyingine nitatumia kwa ajili ya maeneo mengine yatakayojitokeza. Moja katika maeneo muhimu ya Halmashauri yetu ya Madaba ni mapato yanayotokana na vyanzo vya ndani. Moja katika halmashauri changa nchini ni Madaba, Madaba makusanyo yetu ya mwaka hayazidi bilioni moja na hii Waziri naomba kwa kweli anisikilize. Mapato ya ndani ya Halmashauri ya Madaba hayazidi shilingi bilioni moja kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa maeneo ambayo tulitegemea tuongeze mapato walau ku-double ili tupate Bilioni Mbili walau kwa mwaka ilikuwa stendi ya mabasi ya Madaba. Mabasi yote yanayotoka Songea Mjini kuelekea Njombe, kuelea Mbeya, kuelekea Dar es Salaam yanapita Madaba na tathmini yetu mpango biashara wetu unaonyesha, kwa kujenga stendi ya Madaba tutaweza kuingiza walau bilioni moja kwa mwaka na tutaweza kuchangia shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Spika, pale stendi wako wakina mama wenye watoto wadogo mgongoni wanafanya biashara za ujasiriamali lakini mabasi yanashindwa kusimama kwa sababu mazingira siyo rafiki ni hatarishi kwa ajili ya uhai na usalama wa abiria pamoja na wanaoishi maeneo yale. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tumeleta andiko letu sasa ni zaidi ya mwaka, mara ya mwisho nimeulizwa nimeambiwa lipo hazina. Ninakuomba sana wewe ni mchapakazi wewe ni mzalendo tunakufahamu, naomba katusimamie kwenye eneo hili wana Madaba wanasubiri majibu ya Serikali kuhusu stendi hii ili waongeze kipato na waboreshe maisha yao.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nataka niombe Mheshimiwa Waziri Madaba tuna changamoto kubwa sana ya walimu na watumishi wa afya, hizi ajira mpya zinazotolewa naomba sana tuzitazame hizi shule za Madaba na vituo vyetu vya afya na zahanati pamoja na hospitali.

Mheshimiwa Spika, mimi ni mmoja kati ya Wabunge ambao tunachangiana pamoja na wananchi kuwachangia walimu wa kujitolea kwenye shule zetu. Mimi kwa mwaka natumia zaidi ya Milioni Tano kuchangia shule mbalimbali pamoja na wazazi, tunachangia Walimu wanaojitolea ili wapate Shilingi Laki Moja Moja kila mwezi. Zipo shule nyingi ikiwemo Njegea na shule zingine nyingi za Madaba. Tunachangiana fedha kuwawezesha hao walimu waweze kusaidia watoto wetu wasome. Ninaomba hawa Walimu wanaojitolea wafikiriwe kwenye ajira, pia tuongezewe walimu na watumishi wa afya ili tupunguze mzigo kwa wananchi wa Madaba ambao wanachanga fedha kwa ajili ya kuwezesha watoto kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho sijui kama muda utaniruhusu lakini nikuombe sana na naomba hii ninukuu kwenye Taarifa ya Kamati ya iliyokuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria ya Bunge la 12 Mkutano wa 10 naomba ninukuu,

ilishauri Serikali na Bunge lili-adopt walisema hivi “Serikali ibuni utaratibu madhubuti na wenye uwazi ambao utaratibu zoezi zima la ajira Serikalini kwa namna ambayo nafasi zitakazojazwa zitaakisi umoja wa Kitaifa bila kuathiri vigezo” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge wamesema sana na sipendi kurudia ila nataka niwakumbushe Serikali tunapogawa ajira tuangalie uwiano wa maeneo na Mikoa na Majimbo. Tumefanya hivyo kwenye Taasisi za Muungano zote ajira zinatolewa kwa uwiano, Zanzibar na Bara. Tumeangalia kwenye vyombo vya ulinzi na usalama ajira zinatolewa kwa uwiano, tumeangalia kwenye program ya BBT hii ya juzi tu wamewa-appoint vijana kwa uwiano wa Mikoa. Leo tunashindwaje kugawa ajira hizi kwa Watanzania kwa uwiano wa maeneo wanayotoka?

Mheshimiwa Spika, ili tulijenge Taifa tunahitaji Watanzania wote wapate fursa, tusipofanya hivyo hatutaweza kujenga Taifa bora ambalo Watanzania tunalitamani.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu naomba niunge mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kabla sijaenda kwenye hoja zangu, niungane na Waheshimiwa Wabunge ambao wanampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Biteko, pamoja na Naibu Waziri, kwa kufanya kazi vizuri sana katika Wizara hii na kuijengea heshima kubwa sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa utaratibu huohuo, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais ambaye amemuamini Waziri huyu katika sekta hii muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maeneo mawili ambayo ninatamani nichangie kidogo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza linahusu kutumia matokeo ya tafiti mbalimbali za madini ambazo zimefanyika hapa nchini. Zipo tafiti nyingi sana zimefanyika na kubaini uwepo wa madini maeneo mbalimbali. Moja katika maeneo hayo ni Halmashauri ya Wilaya ya Madaba, Mkoa wa Ruvuma. Imechukua takribani miaka zaidi ya 20 kuanza kutumia baadhi ya tafiti ambazo zilifanyika Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Halmashauri ya Madaba miaka 20 baadae baada ya kugundua uwepo wa madini aina ya makaa ya mawe ndipo tumeanza kutumia yale matokeo ya tafiti. Kimsingi tumechelewa sana, leo pengine Madaba tungekuwa mbali sana kiuchumi. Tumeanza kutumia matokeo yale leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri arudi kwenye makabati yake akaangalie matokeo ya tafiti za madini zinazohusu Madaba. Ndani ya Kijiji cha Ifinga katika Halmashauri ya Madaba kuna uwepo wa madini yenye thamani kubwa sana. Naomba kama itakupendeza Mheshimiwa Waziri, na ukiridhika, wasiliana na Dkt. Dalali Kafumu ambaye alishiriki kwenye utafiti huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni utafiti ambao utaleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi kwenye Halmashauri ya Madaba na kwa Taifa katika ujumla wake. Nikuombe sana fanya jitihada za pekee. Binafsi naendelea kufuatilia lakini naomba unisaidie kwenye eneo hilo kwa sababu Wanamadaba wanasubiri kuanza kunufaika na uwepo wa madini hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba uridhie turejee kwenye mradi muhimu sana kwa maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma na Mkoa wa Njombe katika ujumla wake. Lakini manufaa haya hayaishii Njombe na Ruvuma pekee, manufaa ya mradi huu yanakwenda kugusa Tanzania nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi sana, zaidi ya miaka 30, nenda kwenye Hansard za Bunge hili utakuta tunazungumza mradi wa Liganga na Mchuchuma. Tunaposema Liganga – naomba Watanzania waelewe na Waheshimiwa Wabunge tuelewe na tuunganishe nguvu – tunaposema Liganga hii ni deposit ya chuma, chuma inayoweza kujenga reli, inayoweza kuwa malighafi ya kutengeneza magari, inayoweza kuwa malighafi ya kutengeneza pikipiki na baiskeli, ambayo inaweza kuwa malighafi ya kutengenezea nondo na kujengea majengo ya aina yoyote, ambayo inaweza kuwa malighafi ya bati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongelea utajiri huu mkubwa ambao upo ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa inayopakana na Madaba ndani ya Mkoa wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea huu mradi wa Liganga na Mchuchuma, Mchuchuma tunazungumzia makaa ya mawe, Liganga tunazungumzia chuma. Makaa ya mawe ya Mchuchuma yana uwezo wa kuzalisha umeme megawati 600. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyosema megawati 600 Watanzania wanielewe, hii ni zaidi ya nusu ya umeme wote ambao Tanzania ilikuwa nao miaka mitano iliyopita. Kwa hiyo, siyo umeme mdogo, tusiuchukulie mradi huu kitoto kitoto, hebu tuupe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa maana ya multiplayer effect mradi huu mimi ningesema, mradi huu unafuatia kwa umuhimu ukiondoa mradi wa maji wa Bwawa la maji la Mwalimu Nyerere. Ukiondoa mradi wa maji wa umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere mradi unaofuata kwa multiplayer effect na kwa umuhimu wa Tanzania na kwa uchumi wake ni mradi wa liganga na mchuchuma. Mradi huu ulikuwa unaambatana na ujenzi wa reli ya kusini, reli ambayo ingeleta maendeleo makubwa sana kwa nchi hii. Lakini tunapozungumzia mradi huu tunazungumza pia barabara ya lami ya Mkiu-Madaba ambayo ingetumika kusafirisha malighafi ya chuma na makaa ya mawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti,hii miradi yote hatujaipata kwa sababu hatujaamua kuchimba hii chuma. Tumewanyima wana-Ruvuma haki ya maendeleo, tumewanyima haki wana-Njombe kupata maendeleo. Tumewakatalia fursa za ajira watoto wa Madaba, Njombe, Peramiho na Songea Mjini kwa kukataa kujenga mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninamwamini sana Mheshimiwa Dotto, ni mtu wa viwango, amefanya mapinduzi makubwa sana kwenye sekta ya madini lakini anaacha lile jiwe la chuma likae pale kwa miaka mingapi? Nani atakuja kulichimba lile jiwe? Watanzania watasubiri ajira mpaka lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema mutliplayer nyingi sana, sijasema kuhusu aakina mama, akina mama ntilie ambao wangepata ajira kwa kuuza chakula kwenye migodi ya chuma ile. Sijamwambia kuhusu idadi ya vijana ambao wangeajiriwa kwenye miradi ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya sita ilipoingia madarakani kulioneshwa dalili ya kwenda kuanza kuchimba lile jiwe. Na mimi niseme, Watanzani nchi nzima tujue tumekalia utajiri mkubwa sana pale Ludewa; na kama nchi hii haipigi hatua za kutosha ni kwa sababu hatujaamua kutumia malighafi ambazo tumepewa na Mwenyezi Mungu pale Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana uendelee kukazia Serikali na Mheshimiwa Doctor Dotto uko hapa naomba jitahidi kabla Awamu ya Sita hii haijamaliza kipindi chake cha uongozi tuwe tumeshachimba jiwe la chuma la liganga? Tuwe tumeshatoa ajira kwa wana-Ruvuma na Watanzania, tuwe tumeshazalisha malighafi kwa ajili ya baiskeli, magari na vifaa vingine vya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti,baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru wewe kwa kunipa hii fursa ya kuchangia. Kipekee sana, niungane na Waheshimiwa
Wabunge wote waliompongeza sana Mheshimiwa Waziri Ulega kwa hotuba yake ambayo imejaa mikakati mingi na mizuri ambayo imekusudia kuikomboa Sekta hii ya Mifugo na Uvuvi. Vile vile namshukuru na kumpongeza sana Naibu Waziri, Mheshimiwa Silinde na Katibu Mkuu, Mheshimiwa Profesa Shemdoe kwa ushirikiano wao mkubwa ambao wanautoa kwa wadau wa sekta hii na kwa maandalizi ya taarifa makini na yenye mikakati mizuri na mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba, moja katika mipango au mikakati iliyopo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ni kuzalisha au kutengeneza ajira milioni nane, kuanzia mwanzo wa Bunge hili mpaka mwisho wa Bunge hili. Mwanzo wa uhai wa Bunge hili mpaka mwisho wa uhai wa Bunge hili, tunatakiwa tuwe tumeisaidia Serikali kutengeneza ajira milioni nane kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo sekta mama mbili ambazo zinaweza kutengeneza ajira hizo milioni nane au zaidi iwapo Serikali itatusikiliza Wabunge, na iwapo Serikali itapeleka kipaumbele kwa mujibu wa ushauri wa Wabunge. Wabunge humu ndani wameeleza mara nyingi, moja katika sekta muhimu ambazo zitapunguza mlundikano wa watu waliokosa ajira, sekta ambazo zitatuwezesha kupata ajira milioni nane, ni Sekta ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mikakati kwenye kilimo, mikakati mizuri ambayo inawapeleka vijana kuwekeza kwenye Sekta ya Kilimo. Kwa upande wa Mheshimiwa Ulega tumeona mikakati yake ya kutupeleka na kuwapeleka vijana wa Kitanzania wakawekeze kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi. Umewasikiliza Waheshimiwa Wabunge humu, wameeleza mahitaji ya nyama na mazao mengine ya mifugo ndani ya nchi na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale Wabunge ambao wametembelea nchi mbalimbali zikiwemo Ulaya, nchi za Magharibi, waliotembelea nchi za Uarabuni, kote huko wamekiri ndani ya Bunge lako Tukufu Sekta ya Nyama ingeweza kulikomboa Taifa hili. Mahitaji ya nyama nchi za Uarabuni ni kubwa kuliko ambavyo sisi tunaweza kupelea. Nchi yetu imekaa kijiografia, imekaa eneo la kimkakati sana. Kusafirisha ng’ombe walio hai au nyama zenye sifa kupeleka nchi za Uarabuni, kupeleka Comoro ni rahisi kuliko nchi yoyote Afrika ambayo ingeweza kufanya jukumu hilo. Leo tuna maelfu ya Watanzania hawana ajira kwa sababu hatujaamua kuwekeza kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi, pamoja na Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo nchi nyingi ambazo zimejenga uchumi wao kwa kutumia Sekta ya Mifugo na Uvuvi. Nenda Marekani mkaangalie ni asilimia ngapi ya uwekezaji unapelekwa kwenye ufugaji? Leo sisi tulishwe na nchi za Amerika ya Kusini nyama. Fikiria kusafirisha nyama toka Brazil kupeleka Uarabuni na kusafirisha nyama kutoka Tanzania kupeleka Uarabuni, nani anatengeneza faida kubwa zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe, na niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuongeze nguvu kwenye hii sekta. Nasikitika simwoni Waziri wa Fedha hapa. Waziri wa Fedha apeleke fedha Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Tuahirishe mambo mengine ambayo hayana tija, tupeleke fedha kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Nimeitazama mikakati ya Mheshimiwa Waziri hapa, moja katika mikakati mahususi ni uzalishaji wa malisho na ambari kwa maana ya mbegu bora za mifugo. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, Mheshimiwa Naibu Waziri.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mchangia hoja na Bunge lako kwamba kuna kikao cha Baraza la Mawaziri kinachoendelea sasa, ndiyo maana Mawaziri almost karibu wote hawaonekani Bungeni hapa, lakini pia yupo Naibu Waziri wa Fedha. Kwa hiyo, anaposema jambo Wizara ya Fedha, maana yake Naibu Waziri yupo, atalichukua na tutakwenda kulifanyia kazi kama Serikali. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mhagama, unaipokea taarifa?

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana ninaipokea taarifa ya Mheshimiwa Naibu Waziri, na ninatambua kwamba Serikali ipo humu ndani na inasikia na ninaomba inisikilize kwamba hakuna mapinduzi ya uchumi tutayapata Tanzania kama hatupeleki fedha kwenye mifugo na uvuvi. Mikakati ya Mheshimiwa Waziri ni bayana, ipo very clear, kwamba anahitaji kufanya transformation kwenye Sekta ya Mifugo. Kuna eneo la malisho, kuna eneo la mbegu bora. Ukiangalia takwimu alizozileta Mheshimiwa Waziri, haziendi kujibu tatizo. Mheshimiwa Waziri amependekeza kuzalisha malisho hekta 11,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hekta 11,000 ni sawa sawa na tani 55,000 za malisho kwa maana ya hay. Hizi unalisha ng’ombe 25,000 tu kwa mwaka. Tanzania tuna ng’ombe milioni 36,000. Unaona kwamba Waziri ana hamu ya kusonga mbele lakini sisi Serikali tunamkamata miguu. Kwenye hili nimshauri Mheshimiwa Waziri, kwa sababu tunaanza, aachane na biashara ya kwenda kuzalisha hay yeye mwenyewe, isipokuwa fedha hii akaiwekeze kwenye kuzalisha mbegu za malisho. Akazalishe mbegu za malisho hekta 11,000 tupate mbegu za kutosha. Hizi mbegu tuwawezeshe sekta binafsi kuzalisha malisho wao wenyewe. Kwa sababu hizo hekta 11,000 utaenda kutatua tatizo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu, tuanzie hapo. Peleka hii fedha ambayo utapata kwenye hekta 11,000, peleka kwenye mbegu za malisho. Tumefanya kwenye mahindi, tumefanya kwenye maharage, tumefanya kwenye mazao ya kilimo; tumewekeza kwenye uzalishaji wa mbegu, Serikali ihakikishe tunapata mbegu, lakini sekta binafsi ndiyo izalishe, ifanye multiplication ya hizo mbegu. Kwa hiyo, namwomba sana Waziri, hii fedha atakayoipata aipeleke kwenye kuzalisha mbegu. Tuna mahitaji makubwa sana ya mbegu ya brachiaria, haipo nchini, lakini katika mbegu nzuri sana, hay nzuri sana utaipata kwenye brachiaria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shida ya setaria, nimeenda mpaka hapo Iringa, hakuna. Kwa miaka mitatu unasubiri kupata kilo 200 za mbegu. Imagine, nchi hii tupo nyuma sana. Miaka mitatu, minne bado unasubiri upate supply ya mbegu toka kwenye mashamba ya Serikali. Hatuwezi kufanya mapinduzi ya mifugo kama hatutathubutu kuwekeza vizuri kwenye uzalishaji wa mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cenchrus ni mbengu ambayo inafanya vizuri sana hapa Dodoma, lakini nchi hii kuna maeneo mengi yanakuwa makame kama ilivyo Dodoma. Hakuna utafiti uliofanyika Mkoa wa Ruvuma na mikoa mingine kuhakikisha kwamba hii cenchrus ambayo ni resistance kwa mazingira, inaweza ikafanya vizuri kwa maeneo hayo. Mheshimiwa ilete ukaiwekeze huko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasikitika…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mhagama, muda wako umeisha, naomba umalizie.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nilikuwa na mchango kwenye maeneo mengine ya miundombinu na masuala ya chanjo, lakini nitapeleka kwa Mheshimiwa Waziri kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia asubuhi ya leo. Nianze kwa kuungana na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wanampongeza sana Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, Waziri wa Maliasili na Utalii, kwa kazi kubwa, ubunifu na uzalendo mkubwa aliounesha katika utendaji wake Serikalini tangu alivyoanza kuteuliwa kwenye Wizara mbalimbali na sasa kwenye Wizara hii, Mheshimiwa Mchengerwa ameonyesha ubunifu wa hali ya juu sana na mimi nina mpongeza sana huyu Babu yangu kutoka Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane pia na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza Naibu Waziri Mary Masanja, mpambanaji huyu mama, amefika mpaka Madaba na amefanya kazi na Wanamadaba pamoja na Wanawino kwa kweli mchango wake kwa Taifa letu hautasahaulika na hasa kwa Wanamadaba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninayo mambo machache ya kuchangia lakini niliona ni vema nikaanza kuwapongeza na kuwashukuru viongozi hawa wakubwa wa Wizara hii na katika orodha hiyo naomba uniruhusu nimuunganishe na Mkurugenzi Mkuu wa TFS, Dos Santos Silayo ambaye anafanya kazi kwa karibu sana na Mhifadhi Mkuu wa Shamba letu la TFS lililopo Wino, Madaba, kwa uzalendo mkubwa sana waliouonesha kwa wananchi wa Madaba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapompongeza Ndugu Silayo na Dada yetu Glory Kasmiri ambaye ni Mhifadhi Mkuu wa Shamba letu la Wino, ninakumbuka na kutambua mchango mkubwa sana wanaoutoa kwa wananchi wa Madaba. Moja, ieleweke kwamba Mheshimiwa Waziri nadhani unajua kwamba Shamba la Wino la TFS liko katika Halmashauri ya Madaba na shamba lile lina hekta 39,711. Shamba hili linagusa vijiji vitatu muhimu, Kijiji cha Wino, Ifinga na Mkongotema. Kazi inayofanyika kwenye shamba hili ni kubwa na uwekezaji uliofanyika kwenye eneo hili ni mkubwa na shamba hili linaweza likashika nafasi ya tatu hadi ya tano Kitaifa. Kwa hiyo, mnaweza mkaelewa ni ukubwa gani wa uwekezaji umefanyika katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru viongozi wangu hawa kwa kusaidia pia shughuli zingine za maendeleo ambazo wanazifanya kwenye Vijiji vya Wino, Ifinga na Kijiji cha Matetereka. Natambua michango ya cement, natambua mchango wa mabati, natambua mchango wa wajasiriliamali, vifaa vya kuvunia asali lakini mitaji na vifaa vya kufuga nyuki kwenye misitu. Kazi inayofanyika ni kubwa nilitamani niwashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua miche mingi ya miti mnaizalisha na mnagawa kwa wananchi hawa kupitia programu yetu ya panda miti kibiashara, wananchi wa Madaba wamepata miche mingi sana na tunaendelea kupanda, nitumie fursa hii kutoa wito kwa Wanamadaba tuendelee kupanda miti kwa bidii kubwa kwa sababu miaka 10 ijayo Madaba itakuwa moja katika Halmashauri tajiri sana hapa Tanzania, tutakuwa tunafukuzana na Halmashauri ya Mafinga, kwa hiyo niwaalike sana Wanachi wa Madaba kutumia hii fursa ambayo tunaipata TFS kwa ajili ya kuandaa na kukuza uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba pamoja na kazi nzuri ambayo tumeifanya kupitia TFS Madaba, huduma kwa wananchi, tunazo hifadhi na maeneo ambayo yanafaa kuwa hifadhi ya wanyapori. Tumeleta kwako kupata kibali cha kuanzisha Hifadhi ya Wanyamapori Ifinga. Mheshimiwa Waziri naomba nikufahamishe kwamba Ifinga ni Kijiji ambacho kinapakana na Hifadhi ya Mwalimu Nyerere au Selous katika maeneo hayo lakini tunapakana na Malinyi. Tunayo hifadhi kubwa ambayo tulitamani hifadhi hii ichangie kwenye Pato la Kijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki kijiji ni maskini sana ukilinganisha na vijiji vingi Tanzania, ndiyo kijiji pekee ambacho ndicho kijiji na Kata yaani tuna Kata na kijiji kimoja ndicho hicho hicho. Hawa wako mbali sana hawafikiki kirahisi. Tunayo changamoto ya barabara, tunayo changamoto ya kipato cha wananchi, tunayo changamoto ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali. Tumeomba Mheshimiwa Waziri utusaidie eneo hili lina heka 37,225 tunaomba eneo hili litumike kuwa hifadhi ya jamii kwa maana ya WMA. Hatua zote tumezimaliza tunachosubiri ni Wizara yako itume wataalamu wakafanye tathmini ya utoshelevu na mahitaji mengine ya eneo hilo lakini tunaomba sana Mheshimiwa Babu yangu Mchengerwa tupe eneo hili tukafanye hifadhi ya wanyamapori ili kuchangia kipato cha wananchi wetu na kuchangia uhifadhi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba bonde hili linachangia sana maji yanayoenda Rufiji kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. Kwa hiyo, ushiriki wa wananchi katika kuhifadhi maeneo haya kama ambavyo tumefanya kwenye misitu ni ushiriki wa wananchi katika kuchangia kuhakikisha kwamba tunahifadhi Bwawa letu la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Halmashauri ya Madaba inapakana na Hifadhi ya Mbarang’andu, hifadhi hii ipo ndani ya Halmashauri ya Namtumbo lakini kuna Kijiji cha Ngadinda, Kijiji cha Mbangamawe, Kijiji cha Lutukila. Vijiji hivi vyote vinapakana na hifadhi hii na vijiji hivi vyote wananchi wake wameshiriki katika kuhifadhi mazingira ya eneo hili. Tunaomba basi kunapokuwa na gawio linalotokana na mapato ya WMA vijiji hivi vitatu vinufaike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Kijiji cha Ngadinda kimepoteza mpaka miundombinu ya umwagiliaji ambayo ilijengwa kwa ajili ya kuendeleza uchumi wa wananchi wale. Ile miundombinu ya umwagiliaji imeangukia kwenye eneo la WMA na wananchi wanashindwa kulitumia, basi mapato yanayotokana na uhifadhi huo yakasaidie maendeleo ya wananchi wetu wa Ngadinda, Mbangamawe na Lutukila. Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwa maslahi ya muda nikuombe sana hiki Kijiji cha Hifinga kama nilivyokwambia huko nyuma miaka ya 1950 kilikuwa kwenye Wilaya ya Ulanga, kwa hiyo hakikuwa Songea. Sasa kimekuwa adopted Songea kwa sababu ya mazingira yake ya kijiografia. Tumepata wawekezaji kama SUA wana hekta 10,000 za kupanda miti. Tuna KKKT, hawa hawajafanya lolote lakini wana eneo kubwa sana wamelichukua kutoka kwa wananchi. Tunayo program ya FDT Concession lakini tuna Mufindi Wood Poles.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wadau ambao ninawashukuru sana mbele yako nimetamka kuhusu TFS, na Mufindi Wood Poles ninawapongeza sana kwa kuchangia sana maendeleo ya kijiji kile sasa tunajenga kituo cha afya kwa kupitia mchango wa wadau hawa. Ninawashukuru na ninawaomba waendelee, SUA tunawashukuru kwa sehemu wameanza kufanya sehemu fulani lakini bado ahadi zao hazijatekelezwa kwa asilimia 100. Ninaomba ushirikiane nasi kuwataka wadau wote waliowekeza kwenye kijiji cha Ifinga waliochukua ardhi ya kijiji cha Ifinga wakatekeleze ahadi zao na wakapande miti. Kama hawatafanya hivyo Mheshimiwa Waziri tutaomba ushauri wako ili maeneo haya muhimu yarudi kwa wananchi ili waweze kunufaika nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, Mheshimiwa Waziri ninarudia kukupongeza na ninakushukuru sana kwa kupata nafasi hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa kuchangia kwenye Wizara hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nitumie fursa hii kuipongeza kwa dhati kabisa Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kufanya kazi kubwa sana ya miundombinu ya barabara, reli, bandari na viwanya vya ndege. Hatua tunayopiga inatutia moyo sana Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja katika barabara muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Madaba, Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Ruvuma katika ujumla wake ni barabara ya Mkiu – Liganga - Madaba. Barabara hii inatumika na wananchi kwa malengo ya kiuchumi kutoka Wilaya ya Ludewa ndani ya Mkoa wa Njombe kwenda Songea kupitia Madaba Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kwa zaidi ya miaka mitano maelezo yamebaki yale yale kwamba tunafanya upembuzi yakinifu na wa kina. Kazi hii mpaka leo, nimesoma kwenye taarifa za Wizara kwamba upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umekamilika, lakini barabara hii haijatengewa bajeti ya ujenzi wa viwango vya lami. Wananchi wa Mavanga ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa, wananchi wa Mahanje, wananchi wa Ifugwa, wananchi wa Madaba wametutuma tuwaulize Serikali ni lini kwa uhakika barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Waziri, wakati unaendelea kujipanga kutoa majibu haya kwa wananchi hawa niliowataja, kumbuka…

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nilikuwa napenda kumpa taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Joseph Mhagama kwamba barabara hii pia ina umuhimu zaidi; kila siku tunapiga kelele kuhusiana na suala Liganga na Mchuchuma na barabara hii imepita maeneo hayo. Kwa hiyo, Serikali ione umuhimu hasa wa kutengeneza barabara hii kutokana na uzito na unyeti wa mahitaji wa barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mhagama, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Njombe kwa kuniongezea hoja kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ramani ya Tanzania imebadilika, jiografia ya nchi hii imebadilika. Wakati Mwalimu Nyerere anakwenda kuomba fedha Uingereza za kujenga barabara ya Makambako – Songea, Uingereza walimwambia, hatuwezi kujenga barabara from nowhere; by then Songea ilikuwa nowhere, lakini Baba wa Taifa alienda na picha akamwambia Songea, Mkoa wa Ruvuma, Madaba na maeneo mengine ndiko tunakozalisha chakula cha nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, umuhimu wa barabara ile kwa wakati ule ilionekana ni muhimu wa chakula, leo ramani ya Mkoa wa Ruvuma imebadilika. Leo makaa ya mawe yanatokana Mkoa wa Ruvuma, leo Mheshimiwa Neema amesema Liganga na Mchuchuma kuna madini ya chuma kwa ajili ya maendeleo ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri aelewe, tunaposema barabara ya Mkiu – Liganga – Madaba, tunaongeleza uchumi wa Taifa la Tanzania, tunaongelea maelfu ya Wana-Madaba na Wana-Ludewa watakaoajiriwa kama mama ntilie, akina mama watakaoajiriwa kama wafanyabiashara wadogo wadogo katika sekta nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wanaoishi Liganga, wanaoishi Mavanga, wanaoishi Mahanje, wanaoishi Madaba Mjini, hawa wote waliopo pembezoni mwa barabara hizi, wamewekewa ‘X’, wanashindwa kuziendeleza nyumba zao kwa sababu wanaamini kesho barabara itajengwa. Wanaishi maisha ya dhiki, maisha ambayo hayana hadhi ya wananchi wa maeneo hayo kwa sababu wanaamini kesho barabara itajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tukamsaidie Mama Samia Suluhu Hassan kuwafuta machozi wananchi wa Madaba, wananchi wa Ludewa watengenezewe hii barabara ili uchumi wa maeneo yale uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niku-address in a very special way. Huwezi kuongelea maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma kama barabara ya Makambako - Songea haitajengwa kikamilifu. Barabara hii ilijengwa kwa viwango cha chini sana miaka ya 1980 na historia yake nimeisema ndani ya Bunge hili, Baba wa Taifa alienda kuomba msaada Uingereza. Wakati huo Mbunge wa wakati huo kabla hajawa Mbunge, Profesa Mbilinyi ndio alikuwa anabeba mikoba ya Baba wa Taifa. Leo angekuwa hai angewaambieni changamoto alizozipata kupata hii barabara. Leo barabara imebomoka, barabara ina mashimo, barabara haina ubora kabisa, ajali ni kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wanaopita maeneo haya wanapata changamoto ya barabara ya Makambako – Songea. Wananchi wa Igawisenga, wananchi wa Lilondo, wananchi wa Wino, wananchi wa Ifugwa, wananchi Matetereka, wananchi wa Magingo, wananchi wa Lutukila, Ndelenjumba, Bangamawe, wananchi wote wa barabara hii mpaka unafika Likalangiro. Barabara hii nyumba zao zimewekwa ‘X’ wasiziendeleze, wanaishi kwa dhiki sana wakisubiri barabara ijengwe.

MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Ni lini watapata fidia ya barabara zao, ya majengo yao na barabara hii kwa uhakika itajengwa lini? Mheshimiwa Waziri atuambie.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara ile imejengwa muda mrefu sana na ilikuwa imara ndiyo maana imetusaidia kipindi chote hicho, ila sasa hivi imeharibika, ajue hilo msemaji.

NAIBU SPIKA: Actually, ndicho anachokisema hicho. Mheshimiwa taarifa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napokea taarifa nzuri ya Mheshimiwa Dkt. Ntara, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Ruvuma, akiwakilisha Vyuo Vikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Makambako - Songea inahitaji attention ya Serikali kwamba usanifu umefanyika, lakini barabara haijengwi. miaka kwa miaka tunaomba fedha tukaijenge ile barabara. Tukawafute machozi wananchi wanaokaa pembezoni mwa barabara, wakapate fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante Daktari Mhagama.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata hii fursa ya kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye Wizara hii muhimu sana ambayo imebeba maslahi mapana ya Watanzania. Kwanza naomba niungane na wewe na niungane na Bunge lako Tukufu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu na kuwa miongoni mwa viongozi 100 wenye ushawishi mkubwa duniani. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais, tuzo hii anaistahili sana.

Mheshimiwa Spika, pia kuna jambo jingine halijasemwa lakini mimi kwenye kupitia pitia tu mitandao nimeona Mheshimiwa Waziri Stergomena Tax ameonyesha tuzo nyingine ambayo ameipata Mheshimiwa Rais kwenye Pan African Woman Organization, ametambuliwa kama Rais wa kwanza mwanamke katika Afrika Mashariki, Rais mwanamke pekee kwa mwaka 2022 pia kwa kuonyesha uwezo mkubwa wa kufanyakazi kama kiongozi Mkuu wa Serikali. Hayo yote naomba yaunganishwe kama pongezi kwa Mheshimiwa Rais kwa kutambua mchango wake mkubwa kwa maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nilitaka nichangie na niliombe Bunge lako Tukufu litoe maelekezo kwa Serikali linahusu hali halisi ya eneo letu tunalofanyia kazi eneo la Bunge. Upande wangu huu wa kulia tuna barabara ya Dodoma – Morogoro, Waheshimiwa Wabunge wengi wamepaki magari ng’ambo ya pili ya barabara na siku za karibuni kumekuwa na ajali mbalimbali, siku mbili tatu zilizopita pia Mheshimiwa Francis Ndulane alipata ajali pale, yeye ni mmoja katika Wabunge kadhaa ambao wamekuwa wanapata ajali eneo lile kwa sababu ndani ya eneo la Bunge hatuna maegesho ya kutosha, maeneo ya kuegesha magari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia upande huu wa mbele katika geti la Mheshimiwa Waziri Mkuu kuna barabara ambayo inatoka Hazina inakwenda kuungana na barabara ya Morogoro, eneo hilo wanapita watu wa aina mbalimbali lakini Bunge lako Tukufu kwa mazingira yaliyopo na umuhimu wake na Viongozi waliopo humu wanahitaji ulinzi na usalama wa hali ya juu. Lakini pia leo Wabunge wako ili waweze kushiriki kwenye mazoezi ya kujenga afya zao waweze kulitumikia Taifa hili vizuri wanalazimika kwenda nje ya maeneo haya, wanakodi viwanja maeneo mbalimbali ya Mji, eneo hili lingeweza kutosha kwa huduma kama hizo.

Mheshimiwa Spika, zipo hoja nyingi ambazo zinaonyesha kwamba eneo hili la Bunge halitoshi kutoa huduma za kisasa, tunazo changamoto za ofisi za Wabunge, Wabunge hawana ofisi huku, hata wananchi wangu wa Madaba wakija hapa nakutana nao canteen, mimi ni Mbunge nilihitaji nikae nao katika maeneo ambayo tunaweza kuongea masuala ya maendeleo. Kwa hiyo, moja katika mambo yatakayoliwezesha Bunge lako Tukufu kufanya kazi vizuri ni kuwa na mazingira rafiki salama yatakayowafanya Wabunge wafanye kazi kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninatambua hatua ambazo Bunge limefanya moja ni kwamba limejaribu kutathmini na kuthaminisha maeneo haya ya Bunge yenye majengo na viwanja vilivyo wazi. Hiyo kazi najua Bunge wamemaliza lakini niiombe Wizara sasa ichukue jukumu hili la kuisaidia Bunge kwa haraka zaidi kuyapata hayo maeneo ili tuweze kuwa na Bunge la kisasa linaloweza kutoa huduma bora kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, naelewa tupo kwenye hatua za mwisho za kupitisha bajeti yawezekana jambo hilo kibajeti halijakaa vizuri. Bunge lako lina mamlaka linaweza kuitisha Kamati ya Bajeti ikakaa na Serikali tukafanya amendment ambazo zitaruhusu kuingiza hizo bajeti za kumaliza hili tatizo ambalo litaenda kuboresha utendaji wa Bunge lako na hivi Watanzania watapata huduma bora wanazozihitaji, hilo lilikuwa ombi langu la pili.

Mheshimiwa Spika, ombi la tatu kama kuna Wizara imeweza kuitikia wito wa Watanzania kuhusu migogoro mbalimbali ni Wizara hii ya Ardhi na hizi credit zimwendee kwanza Mheshimiwa Waziri wa sasa, Dada yangu Mheshimiwa Angelina Mabula, pia mtangulizi wake Mheshimiwa Lukuvi, kwa kweli hawa wamefanyakazi kubwa sana nchi hii. Mimi nimepata bahati ya kuhusika katika kupanga na kuleta majina ya watu watakaozungumza kwa mara ya kwanza nimeona mapendekezo machache sana ya watu wanaotaka kuongea kwenye Wizara hii, kwa sababu migogoro mingi imetatuliwa na Serikali kupitia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninampongeza sana mtangulizi wake Mheshimiwa Mabula, yeye mwenyewe Mabula na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Ridhiwani wanafanyakazi nzuri sana. Ninazo salamu mahsusi toka Madaba wananchi wa Madaba walipomuona Mheshimiwa Mabula ameenda Mbeya walivyomuona ameenda Mwanza walivyomuona ameenda maeneo mbalimbali akitatua migogoro ya wananchi wakasema tunatamani Mheshimiwa Waziri aje na Madaba kwa sababu wanayo imani nae sana.

Mheshimiwa Spika, migogoro ya ardhi haiwezi kuendelea kutatuliwa na Mahakama pekee, Mahakama zina utaratibu ambao unachelewesha sana, tujifunze kwa Mzee Lukuvi wakati ule anakwenda ndani ya Mkoa, anakaa na wananchi anatatua mgogoro mpaka leo hatujasikia kelele katika maeneo hayo. Huduma kama hii kwa Madaba na Mkoa wa Ruvuma bado hatujaipata kikamilifu. Mheshimiwa Waziri ninakuomba wananchi wanayo imani kubwa sana na wewe, wananchi wanaimani kubwa sana na Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan, wananchi wanayo imani sana na Watendaji wako wanaamini ukiendelea kwa mwendo uleule Tanzania hii migogoro itapungua kwa kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Spika, sehemu kubwa ya migogoro ambayo utaikuta kwenye maeneo yetu inachangiwa na taasisi zingine za Serikali, mimi ninaamini dhamana ya ardhi imekabidhiwa Wizara ya Ardhi hii ni Wizara ya kisekta. Mwananchi mwingine yeyote na idara nyingine yoyote na Wizara nyingine yoyote ya Serikali ni watumiaji wa ardhi, wana mamlaka sawa kama mwananchi mwingine mwenye ardhi. Pale inapotokea mwananchi ana matumizi na ardhi, Serikali kupitia Idara zake wanaihitaji hiyo ardhi basi Wizara ya Ardhi isimame kama Hakimu anayetenda haki kwa kila pande. Madaba tuna mgogoro wa ardhi kati ya wananchi wa Kipingo na watu wa hifadhi lakini watu wa hifadhi wametumia ubabe kuchukua maeneo ya wananchi, utaratibu huu hauwezi kuleta afya.

Mheshimiwa Spika, wewe unajua Mheshimiwa Rais ni kipenzi cha watanzania wanyonge, ni Mama mpenda haki hataki kuona Mtanzania yeyote anaonewa ndani ya nchi hii, Mama Mabula naomba endelea kumsaidia Mheshimiwa Rais kuwasimamia wananchi kupata haki zao za ardhi wakiwemo wananchi wa Kipingo, wananchi wa Ngadinda, wananchi wa Mkongotema, wananchi wa maeneo yote ya Madaba na Mkoa mzima wa Ruvuma na Tanzania katika ujumla wake.

SPIKA: Sekunde 30, malizia sentensi.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi siku za karibuni dunia na Taifa letu kumekuwa na shock kubwa sana ambayo imepelekea upandaji mkubwa sana wa bei ya bidhaa muhimu kiasi ambacho Watanzania lakini na wananchi wengi duniani wamepata ugumu wa kukabiliana. Kama Taifa lakini kama Serikali ukilinganisha na Serikali zingine zote duniani moja katika majukumu yao muhimu katika eneo hili ni kuhakikisha kwamba inafanya intervention ambayo itasaidia kupunguza gharama za maisha itasaidia kupunguza upandaji wa bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu unaonyesha moja katika bidhaa ambazo zina madhara makubwa sana kwenye upandaji wa bei ya bidhaa na huduma katika nchi yoyote ni mafuta ya petrol, diesel na kadhalika. Changamoto hii bado tunayo na kwa sehemu imepata utatuzi kulikuwa na sera za kifedha na za kikodi ambazo Serikali ilizifanyia kazi na tukapata ruzuku na sasa tumeona faida yake kwamba mafuta kwa sehemu kubwa yamepungua bei ukilinganisha na vile ambavyo ingekuwa kama Serikali isingechukua hatua hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili naomba niipongeze sana Serikali imechukua hatua muhimu lakini niombe sana hatua hizi zisiishie kwenye ruzuku peke yake, mikakati mingine yote ambayo Serikali imeiweka ikiwemo pamoja na Strategic Reserve iendelee ili Watanzania waweze kupata nafuu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni ule ule kwamba gharama ya maisha imepanda duniani kote, bei ya nishati imepanda duniani kote kinachotofautisha kati ya Taifa moja na lingine ni hatua ambazo Serikali inazichukua ili kupunguza gharama hizo. Tanzania tumeongoza njia Mheshimiwa Rais ameongoza njia kwa kutoa hizo Bilioni 100 ambazo zimekuja kama ruzuku kwenye sekta ya mafuta ili Watanzania wapate unafuu. Unafuu huu utapatikana zaidi iwapo jitihada zingine ambazo Mheshimiwa Waziri umezisema utaendelea nazo na utaenda kuzikamilisha na mimi nitaunga mkono hoja ya bajeti hii kwa sababu naamini watakwenda kuitekeleza hii mikakati ambayo imewekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kuhusu Jimboni kwangu. Naishukuru Serikali, kwa sehemu Madaba tumepiga hatua kwenye upatikanaji wa umeme vijijini, asilimia karibu 95 ya Vijiji vya Madaba na maanisha Madaba kama Halmashauri, vijiji vyote vimepata umeme isipokuwa Kijiji kimoja cha Ifinga. Kwenye hili naipongeza sana Serikali. Kijiji kilichobaki ambacho ni Ifinga kipo kilometa 48, Mheshimiwa Waziri alituletea wataalam wa masuala ya umeme hapa na wakandarasi, tumezungumza nao na wametuhakikishia kwamba mwezi Desemba, Kijiji cha Ifinga kitakuwa kimepata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wanaifinga wanasubiri Desemba waende kusherehekea Krismasi wakiwa na umeme kwenye nyumba zao. Pia pamoja na jitihada nzuri za Serikali, yapo baadhi ya maeneo ndani ya Madaba hayajafikiwa na umeme, nayo ni maeneo muhimu sana. Kwanza tunazo sekondari mbili, hizi naomba Mheshimiwa Waziri aziandike tafadhali, tunayo Sekondari Kongwe ya Lipupuma, ipo ndani ya Kata ya Mkongotema, Kijiji cha Mkongotema, sekondari hii ni ya muda mrefu wakati wana-design umeme sekondari ilikuwepo, wakati wanaleta nguzo sekondari ilikuwepo, wakati wanafunga nyaya sekondari ilikuwepo, lakini hadi leo haijapata umeme na mtaa mzima wa Lipupuma haujapata umeme. Watanzania wanaoishi maeneo yale wana imani na Mheshimiwa Waziri, tunaomba tupate umeme haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Madaba pia kuna sekondari mpya inajengwa pale na sekondari hii amepewa heshima Mbunge wa Jimbo la Madaba, Joseph Kizito Mhagama na inaitwa kwa jina hili. Tunaomba tupewe umeme haraka sana kwa sababu mwezi Januari tunaanza masomo pale. Kwa hiyo tunaomba sana eneo hili lipate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo eneo la sekondari mpya vile vile inayojengwa Maweso, ni pembezoni kidogo cha kijiji, hatuna umeme. Watanzania wanaoishi eneo lile wanasubiri wapate umeme. Maeneo ambayo yamesambazwa umeme kwenye vijiji vyetu hayajasambazwa kwa ukamilifu. Tunaamini kwenye programu ya kujaziliza umeme na kupanua umeme, Madaba itapewa kipaumbele. Kijiji cha Mtepa mitaa yake mitatu Mtumbika, Makaraveti na Miembeni kote umeme haujafika. Wananchi hawa wanategemea Waziri awape kipaumbele

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Vitongoji vya Ngadinda, Lilondo na baadhi ya vitongoji vya Mahanje havijapata umeme. Hata Madaba Mjini pale pale katikati ya mji kuna vitongoji havijapata umeme, Kijiji cha Gumbilo, kijiji Kongwe kabisa nacho baadhi ya vitongoji havijapata umeme. Mimi binafsi sina mashaka juu ya commitment ya Serikali kwenye kupeleka umeme vijijini, naelewa jambo hili lina bajeti implication, lakini kwa sababu tulishawaahidi Watanzania na kwa sababu mama amedhamiria kufanya kazi hii kwa weledi mkubwa, naomba Wizara imsaidie mama kufikisha umeme vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kukuza uchumi kama hatutafikisha umeme vijijini ili vijana wa Kitanzania waweze kujiajiri kwenye shughuli ndogo ndogo za ufundi umeme, ufundi simu, ufundi redio, lakini wafanye masuala ya welding. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maslahi ya muda, nakushukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Madaba na naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kukushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia. Pia nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na siha nzuri kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia Muswada muhimu sana, Muswada ambao kama utasimamiwa utageuka kuwa sheria na utasimamiwa vizuri, utatutoa Watanzania toka hapa tulipo na kutufikisha Tanzania bora zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kueleza na namna ambavyo Muswada huu wa haki ya kupata taarifa. Chimbuko la Muswada huu ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama ambavyo wengi wameeleza, Ibara ya 18(d) kila mtu ana haki ya kupata taarifa. Kwa hiyo, Muswada huu misingi yake ni universal law na misingi yake ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wale ambao wanabeza Muswada huu wanaikosea haki Katiba ya Tanzania na wanawakosea haki Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona vema pia nieleze kidogo historia ya Muswada wenyewe. Kama ambavyo tayari imeelezwa hapo awali, Muswada huu haujatunguliwa tu hewani, mpaka mwaka 2005 nchi 66 duniani zilishapitisha sheria hii, toka mwaka 2005 nchi 66 wana-practice sheria hii katika nchi zao. Sheria hizi katika nchi mbalimbali zinaweza zikawa zinatofautina kwa majina lakini maudhui ya sheria hii katika hizo nchi zote 66 ni ambayo kwa sehemu kubwa yanafanana na maudhuhi ya hii sheria ambayo tunataka tuipitishe. Hivyo, ni vizuri wale ambao tunabeza hii sheria hebu tujikite pia kwenye historia na tujaribu kuangalia comparative studies za hii sheria zinasemaje na practice za nchi zingine wamewezaje ku-practice.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii kwa hapa Tanzania imechelewa sana kufika. Nchi ya Sweden tayari walishaanza ku-practice sheria hii mwaka 1766, ni miaka mingi sana iliyopita. Leo Tanzania tunashangaa huu Muswada ni ajabu sana!
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kueleza kidogo historia ili tuweke kumbukumbu zetu vizuri, napenda pia nileleze relevance; mantiki ya huu Muswada. Muswada huu kwa namna ulivyo una mahusiano ya kiutatu na mambo matatu; moja ni uwazi, pili ni uwajibikaji na tatu ni maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa taarifa, utoaji wa taarifa unaleta uwazi na panapokuwa na uwazi unazaa uwajibikaji. Mtumishi yeyote wa umma au mtumishi yoyote wa sekta binafsi, sekta ambayo ina maslahi ya umma pale atakapoona kwamba taarifa zake zinatakiwa ziwe wazi ataongeza sana uwajibikaji, pia kwa kuongeza uwajibikaji dhana nzima ya kuwaletea Watanzania maendeleo itakamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naona relevance kubwa sana ya Muswada huu kufika wakati huu katika Bunge lako Tukufu na niwaombe Waheshimiwa Wabunge tukiulewa Muswada huu katika muktadha huo, kwa hakika tutawatendea haki Watanzania kwa kupitisha kwa kuunga mkono Muswada huu kwa asilimia mia moja. Kwa sababu kwanza unaenda kuleta uwazi, unaenda kuongeza uwajibikaji kwa taasisi zote za umma na binafsi zinazogusa maslahi ya umma, lakini pia kwa kuleta uwajibikaji tunakwenda kupata maendeleo zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshangaa sana katika Serikali hii ya Awamu ya Tano ambapo tunataka kupiga hatua kubwa ya maendeleo kama tungeweza kwenda bila kupata sheria hii. Hata hivyo, nina mapendekezo ya maboresho kwenye Muswada. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza la mapendekezo linajikita kwenye taarifa zilizozuiliwa Ibara ya 6(6) ya Muswada huu. Ibara ya 6(6) inasomeka kama ifuatavyo:-
“Mtu yeyote anayetoa taarifa iliyozuiliwa kinyume na mamlaka ya umma, kinyume cha sheria hii anatenda kosa na endapo atatiwa hatiani atatumikia kifungo kisichopungua miaka 15 na kisichozidi miaka 20.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia makosa yaliyoainishwa katika Ibara hii yanatofautiana sana. Naona kwamba yale makosa ambayo yana maslahi makubwa kwa usalama wa nchi yetu, yanagusa moja kwa moja eneo la usalama, makosa haya yasiwe na adhabu mbadala isipokuwa adhabu ambayo imependekezwa katika Ibara hiyo. Makosa ambayo hayana athari kubwa kwa usalama wa Taifa letu basi yatafutiwe adhabu mbadala au adhabu ipunguzwe. Kwa hiyo, napendekeza kwamba haya makosa yawekwe kwenye mafungu mawili kulingana na uzito wake na kutegemeana na athari ambayo itakuwa kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nahofia kupendekeza adhabu hii ipunguzwe kwenye Ibara ya 6(6) tena kwa sababu kuna tabia ya watu waovu wanaolitakia Taifa letu balaa wanafanya makosa haya na wakishahukumiwa Mahakamani kulipa faini ya pesa wanakwenda mtaani wanachangishana pesa wanaenda kulipa faini. Tusiruhusu jambo hili kwa jambo ambalo lina maslahi mapana kwa Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ambayo napenda nichangie ni wajibu wa kutangaza taarifa, Ibara ya 9. Ibara ya 9 inasema kila mmiliki wa taarifa siyo zaidi ya miezi 36 baada ya kuanza kutumika kwa sheria hii, baada ya kuombwa atatoa kwenye gazeti, tovuti au gazeti linalopatikana kwa wingi likiwa na maelezo hayo mengi hapo chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufikia maendeleo kama nilivyosema katika utangulizi wangu tunahitaji Serikali yenye uwazi na uwajibikaji. Palipo na uwazi na uwajibikaji ndipo tutapata maendeleo. Iwapo tutaacha kipindi hiki cha miezi 36 maana yake miaka mitatu kutoka sasa ni muda mrefu sana. Tutashindwa kujipima katika kipindi hiki cha miaka mitano. Ushauri wangu eneo hilo nalo liboreshwe kwa kuweka kipindi kifupi inavyowezekana ili kukidhi haja ya kupata Serikali yenye uwazi, uwajibikaji na hatimaye kufikia malengo ya maendeleo tuliyojipangia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo niliona nichangie ni Ibara ya 11(1) na Ibara zote zinazoendelea Ibara ya 12, 13, 14 mpaka 16. Ibara hii ya 11(1) inaeleza kuhusu notice pale ambapo ombi la kupewa taarifa linapowasilishwa. Ipo haja, tumeona na tunaishi katika jamii hii ya Kitanzania tumeona mara nyingi unakwenda katika ofisi zetu za Halmashauri, unakwenda kwenye Wizara na unakwenda ofisi za Kijiji kuomba taarifa kwa barua, lakini unazungushwa miezi mitatu, minne. Kipindi cha siku 30 kilichopendekezwa hapa ni kirefu sana kwa taarifa ambazo tayari zipo mikononi mwa wamiliki wa taarifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu yangu Ibara hii ya 11 mpaka Ibara ya 16 zifanyiwe maboresho ili kuakisi haja nzima ya kupata taarifa kwa muda mfupi inavyowezekana. Naamini nikileta barua katika Halmashauri ya Wilaya, nataka taarifa ya maendeleo ya mradi „A‟ haitakiwi ichukue zaidi ya siku mbili kunitaarifu kwamba barua hiyo wameipokea na sitegemei ichukue zaidi ya siku saba kunipa hizo taarifa. Zipo tayari good practices katika Serikali yetu. TAMISEMI nimeona wana service charter, ile service charter inaweza ikawa model kwa Wizara, lakini pia inaweza ikawa model kwa maeneo mengine yote ambayo yanatakiwa kutoa taarifa. Imeelezwa vizuri ni lini unataarifiwa kwamba barua yako ya kuomba taarifa imefika na ni lini unapewa taarifa. Kwa hiyo, kila kitu kimeelezwa hivi, hata anayeomba taarifa anapolalamika angalau anakuwa na kitendea kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anatunga Kanuni za utekelezaji wa sheria hii basi aangalie hicho kipengele ambacho kitaboresha na kitaharakisha utoaji wa taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana lakini niweke tu tahadhari kwamba watu wasitudanganye na wasiwadanganye Watanzania kwamba sheria hii inakwenda kuondoa haki za Watanzania na kwenda kugandamiza haki za Watanzania. Ni makosa makubwa sana kuoanisha haki ya kupata taarifa na haki ya habari ni vitu viwili tofauti japo vinafanana. Haki ya kupata habari siyo synonym ya haki ya kupata taarifa. Ni vema wakajikita kwenye historia ya nchi mbalimbali wakajua nchi zinavyo-practice hii sheria na sisi namna ambavyo tuta-practice ni vizuri tukashauriana namna nzuri ya kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali, 2017
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia Muswada huu muhimu sana kwa maslahi ya Watanzania. Lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Muswada huu ukiuangalia ni Muswada ambao unatoa fursa pana kwa Serikali kuongeza ufanisi katika utendaji wake. Katika mfumo wa kawaida wa kiutendaji kwa Waheshimiwa Wabunge ambao mna uzoefu kidogo wa kufanya kazi na taasisi kubwa utagundua kwamba, kunakuwa na taarifa za aina mbili; kuna taarifa za menejimenti, lakini kuna taarifa za governance.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika level ya menejimenti ni taarifa ambazo zinatolewa katika ngazi ya taasisi husika katika muda wa miezi mitatu, ili kuiruhusu menejimenti iweze kujitathmini na iweze kuji-re-orient kufuatana na mahitaji na hali halisi ya wakati ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini unapokuja kwenye level ya governance taarifa ile inatakiwa kwa kweli iwe imeshiba kidogo na iwe imejitosheleza kwa maana ya kwamba hata menejimenti yenyewe imepata nafasi ya kujitathmini na kuji-orient ili kuendena na malengo yaliyokusudiwa.

Sasa sisi Waheshimiwa Wabunge ni level ya juu sana ya utendaji wa Taifa hili. Katika mfumo nilioueleza sisi Wabunge tungejiweka katika level ya governance. Sasa tunapotaka kupata ripoti kila miezi mitatu ni kama vile ambavyo tunajiweka kwenye level ya menejimenti on daily basis. Kwa hiyo, mimi nikubaliane kabisa na Serikali kwamba kwa Muswada huu sasa haya mapendekezo yanayoletwa kwenye hizi sheria yakubaliwe na Wabunge na yaweze kuboresha utendaji wa Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Sura ya 439, Ibara ya 4 mpaka ya 11 nimeshangazwa kidogo na Hotuba ya Kambi ya Upinzani inayotutaka sisi Wabunge au sisi kama Taifa tuwe sawa na mnyama anayeitwa nyumbu! Ukienda katika mbuga za wanyama kuna wanyama wawili, wale mtakaobahatika kwenda katika mbuga za wanyama kujifunza kidogo, kuna aina za wanyama wawili ambao wanaweza kukupa somo zuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mnyama anaitwa nyumbu na kuna mnyama anaitwa nyati. Ukikutana na nyati anasafiri, anasafiri na kundi, katika kundi wanakwenda, wanasimama, wanaangalia mbele, wanaangalia nyuma, wanajipima, wanatafakari, wanasahihisha makosa, wanapiga hatua wanasonga mbele. Lakini ukimkuta mnyama nyumbu ameamua kwenda, basi atakwenda hata kama kuna makorongo, hata kama kuna nini, atatumbukia ataendelea na safari.

Sasa sisi Wabunge sio nyumbu, tumetekelza mfumo huu wa zamani wa quarterly reports, tumejifunza changamoto zinazotokana na mfumo huu, kwa sehemu kubwa Serikali imetumia muda mwingi kukaa kuandika ripoti kuliko kutekeleza majukumu waliyotumwa na Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejifunza nini katika huo mfumo; ufanisi wetu ulikuwa mdogho sana. Leo tumekaa tumeona hilo tatizo tunaamua kuli-focus, tunapoli-focus tunabadilisha huo mfumo tuiache Serikali ifanye kazi na menejimenti, wajipime wao ndani ya taasisi zao kwa miezi mitatu, halafu waende tena miezi mitatu, baada ya miezi mitatu mingine watuletee hapa ripoti iliyoshiba na inayojitosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshangazwa kwa taarifa ya Upinzani wanasema mamlaka ya Bunge yamepunguzwa. Lazima tutofautishe kati ya mamlaka na ufanisi. Mamlaka yanakuwa na tija tu pale ambapo pana ufanisi mzuri wa kazi. Sasa kama mamlaka yako wewe kama Bunge yana-compromise ufanisi katika Serikali, mamlaka yako yanakuwa hayana tija, ya nini! Hatuwezi kubaki kwenye mamlaka kama mamlaka hayo hayaisaidii Serikali kutekeleza wajibu wake na kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napenda niwakumbushe wenzangu Kambi ya Upinzani, marafiki zangu kwamba, kama kuna sababu za msingi Bunge hili linaweza kuitisha taarifa yoyote toka Wizara yoyote wakati wowote. Mamlaka hiyo ipo na itaendelea kuwepo na mabadiliko haya hayaendi kuondoa hayo mamlaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuu sana na ninaunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 5) wa Mwaka 2017
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa hii nafasi. Pili nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuwa mmoja katika wachangiaji wa kwanza kabisa wa Muswada huu muhimu sana wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 5 wa mwaka 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefuatilia kwa makini sana mawasilisho yaliyofanywa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, pia na Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria. Pia nimebahatika kusoma mambo mbalimbali ili nione namna gani naweza nikaishauri Serikali kwenye jambo hili mahususi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niipongeze sana Serikali yetu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli. Ukisoma Muswada huu unapata picha iliyo dhahiri kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga vizuri sana kurudisha rasilimali za Watanzania mikononi mwa Watanzania na kuwajenga Watanzania kiuchumi. Sheria ya Ardhi, Sura namba 113 marekebisho yaliyoletwa hapa yanalenga kwenda kulinda rasilimali ardhi ambayo kwa sehemu kubwa imetumika vibaya sana na watu wasioitakia mema Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Sheria hii sitachambua maeneo mengi kwa sababu nataka nijikite kwenye eneo lingine, lakini niwashawishi Waheshimiwa Wabunge tuipitishe kama ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo nataka kwa muda mfupi niliopewa nijikite zaidi ni kwenye hii Sheria ya
Utumishi wa Umma, Sura 298. Ukisikiliza mawasilisho yaliyofanywa unapata picha dhahiri kwamba katika kipindi fulani tulijisahau kidogo kuweka ajira za kutosha kwenye eneo hili mahususi kabisa linalogusa Wahadhiri wa Vyuo Vikuu lakini na Madaktari. Matokeo yake leo tuna upungufu mkubwa sana wa kada hiyo. Kati ya mwaka 2012 mpaka 2015 watumishi katika kada hiyo waliofikia umri wa kustaafu walifika
395. Katika kipindi hicho hicho Serikali ililazimika kuingia mkataba na watumishi hao hao waliostaafu na kufikia idadi ya 324.

Sasa unapata picha kwamba waliofikia umri wa kustaafu 395 wanaoombwa kurudi kuendelea na majukumu 324 sawa sawa na asilimia 82. Sasa huu ni ushahidi kwamba kada hiyo ina upungufu mkubwa sana wa watu. Sasa Serikali imechukua hatua hiyo kwa muda mrefu, imeendelea kuwa- retain wale waliostaafu kwa asilimia 82.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhara yake ni matumizi makubwa ya fedha za Serikali, hawa watumishi wanapostaafu wanalipwa mafao yao yote, wanapewa stahiki zao zote ikiwemo kiinua mgongo. Tunapowaomba sasa warudi kazini kuendelea na kazi tuna-negotiate upya mikataba na masharti yanakuwa mapya wakati mwingine, na gharama pengine zinakuwa kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi wanapomaliza kipindi, kila kipindi cha miaka miwili kinapoisha sasa Serikali inalazimika kuwalipa tena gratuity ambayo kimsingi ni kubwa sana. Ukisoma katika makabrasha mbalimbali katika kipindi cha miaka miwili tu Serikali imetumia zaidi ya bilioni 2.9. Sasa kimsingi hizo ndizo hoja za msingi ambazo binafsi naziona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine kubwa inahusu gharama ambazo Serikali inatumia kuwekeza kwenye kuijenga hiyo kada. Hawa Madaktari na Maprofesa, Wahadhiri na Madaktari Bingwa ni kada ambayo ni rare sana katika Taifa lolote. Fedha inayotumika kuwafikisha hapo ni kubwa sana, lakini pia muda tunaotumia kuwajenga na kuwaelimisha ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Profesa wa kawaida wengi wanafikia nafasi hiyo wakiwa na miaka 35 hadi 50 na muda wa kulitumikia Taifa unabaki labda miaka mitano, kitu ambacho ni hasara kubwa kwa Watanzania lakini pia hasara kubwa sana kwa Taifa. Pia gharama za kumsomesha daktari bingwa mmoja tu na taaluma hizi hapa hatuna, tunawapeleka nje ya nchi, ambapo UK peke yake inagharimu milioni mia moja thelathini na tisa, ni kiasi kikubwa sana cha pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Wahadhiri wa vyuo vikuu, wale ambao tunataka waweze kuwapeleka vijana wetu kwenye soko la ushindani wa ajira kwa nchi ya Uingereza peke yake inagharimu milioni themanini na nane kumpata mtaalam mmoja mwenye hizo sifa. Kwa hiyo, unaona ni uwekezaji mkubwa sana ambao mtu binafsi anaufanya lakini pia Serikali inaufanya. Itakuwa si jambo la hekima na la busara kuifanya hii rasilimali watu ambayo tunaijenga kwa muda mrefu itumike katika muda mfupi tu kwa maslahi makubwa ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna maeneo ambayo tunaweza tukajifunza; sisi Watanzania si watu wa kwanza kufikia maamuzi kama hayo. Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria ameeleza bayana, ametupa mifano, kwamba Nigeria muda wa kustaafu miaka 70 kwa hiyari lakini anakwenda mpaka miaka 75, nchi jirani ya Kenya miaka 70 kwa kada kama hiyo. Nchi zingine ambazo zimeendelea zaidi Ujerumani hata Uingereza hawana kipindi cha kustaafu inategemea uwezo wa mhusika lakini pia mahitaji ya kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, hiyo ni kada ambayo tukiziondoa na kada zingine zote ambazo zina haki sawa katika Taifa, hii ni kada adimu sana kuipata katika historia ya nchi yetu na ndiyo maana unaona wanatoka, wanamaliza watu 395 wanarudishwa kazini watu 324 asilimia
82. Kwa hiyo, naunga mkono hoja kwamba huu Muswada upite ili taifa letu liweze kunufaika na rasilimali watu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kwa Serikali ni hii, tunakwenda, naamini Waheshimiwa Wabunge tutakubali kuipitisha na sasa itakuwa sheria, lakini ni vyema sasa Serikali tukaja na mkakati mahsusi kabisa wa kupunguza hili tatizo. Hii ni kwa sababu kuna Watanzania wengi wanakosa fursa kama hizo kwenye maeneo mbalimbali. Hatua ambayo Serikali inaichukua kwanza itajenga motisha kwa vijana kuwekeza katika elimu ili waweze kuwa madaktari bingwa lakini pia wafikie hadhi ya uprofesa katika shughuli zao, itawapa hiyo motisha. Pia Serikali sasa ije na succession plan ya eneo hilo la elimu na eneo la afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ndio ulikuwa mchango wangu wa leo. Nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa Mwaka 2018
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia muswada ambao ni muhimu sana kwa demokrasia, amani na utulivu wa Taifa letu. (Makofi).

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kuleta muswada huu mahususi ambao unakwenda kulijenga Taifa lenye nidhamu, demokrasia, amani na utulivu; na sifa hizo zote zitabaki sifa za kudumu kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili naomba nieleze masikitiko yangu. Kambi ya Upinzani imetumia muda mrefu sana kwenye jukwaa lako na ndani ya Bunge hili tukufu kupotisha umma. Hotuba nzima ya Kambi ya Upinzani ukiisikiliza au wanapotosha kwa makusudi Watanzania au hawajauelewa huu muswada. Sasa mimi naomba nifanya assumption kwamba wenzetu Kambi ya Upinzani hawajauelewa huu muswada na nichukue jukumu la kizalendo kabisa la Mtanzania anayewajibika katika Taifa lake kuufafanua huu muswada, hasa maeneo yale muhimu ambayo nimeona yamepotoshwa kwa makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya manufaa makubwa ambayo muswada huu unayaleta kwetu na kwa Watanzania wote ni dhana ya uwazi na uwajibikaji, kwa lugha ya kigeni tungesema transparency and accountability. Hizi dhana nilizozizungumza hapa unaziona kwenye Ibara ya 21 ambayo inataka vyama vyote vya siasa vitoe tamko la mali na madeni ya taasisi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Ibara ya 22 kuhusu dhana ya uwazi na uwajibikaji kwa vyama vya siasa inavitaka vyama vya siasa viwe na Afisa Masuuli (Accounting Officer) na Ibara ya 23 katika hiyo dhana ya uwazi na uwajibikaji inavitaka vyama vya siasa viwe na akaunti maalum ambayo itatumika kwa ajili ya kuhifadhi fedha za ruzuku. Ibara ya 25 kwenye hiyo hiyo dhana ya uwazi na uwajibikaji inamtaka mkaguzi Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) akague hesabu za vyama vyote vya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya naomba niyafafanue, hii dhana ya uwazi na uwajibikaji na Watanzania wajue kwamba wenzetu ambao walikuwa wanaendesha vyama vya kisiasa kwa mfumo wa ukanjanja, kwa mfumo wa udanganyifu, wenzetu baadhi yao wamekuwa wanavitumia vyama vya siasa sio kama taasisi za kwenda kuijenga nchi isipokuwa kama SACCOS ili waweze kujinufaisha na fedha za ruzuku. Fedha hizi Serikali imetambua kwamba, ni fedha za Watanzania; fedha hizi zinapatikana kwa kupitia kodi. Hii ruzuku inayopelekwa kwenye vyama vya siasa lazima isimamiwe, na ndiyo mantiki ya kuleta muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tusiupotoshe umma kuhusu jambo hili. Hili linakwenda kuwasaidia Watanzania, fedha zao na kodi zao zinakwenda kusimamiwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nimeliona linapotoshwa, lakini limebeba maudhui muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu ni Ibara ya 5(5)(A)(1). Ni kuhusu uratibu wa elimu ya uraia na programu za kujengea uwezo vyama vya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe unajua vizuri kwamba hata shule zetu tunazipelekea curriculum, wanachofundishwa tunakijua, tumekisimamia. Vyama vya siasa ni matanuru ya kupika viongozi, hawa viongozi wakishaiva katika chama ndio wanaokwenda kuliendesha Taifa hili. Kwa hiyo, haki na wajibu wetu kama Watanzania ni kujiridhisha juu ya maudhui ya mambo yote ambayo yanakwenda kwenye vyama vya siasa ili yale yanayokwenda kufundishwa katika vyama vya siasa yaendane kwanza na utamaduni wetu, yalandane pamoja na mila na desturi zetu za Kitanzania. Dunia yetu imebadilika, values zetu hazifanani hata kama nchi zetu ni za kiafrika bado kuhusu tunu tunatofautiana, values zetu zinatofautina. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata katika imani tunu zetu zinatofautiana. Mataifa haya tunu zao zinatofautiana, tunazo mila, tunazo tamaduni zetu na tunazo desturi zetu hizo lazima tuzisimamie kufa na kupona. Kwa hiyo, muswada huu unakuja na hiyo kwamba, mtu yeyote au taasisi yoyote, iwe ya ndani au iwe ya nje, itakayokwenda kutoa elimu ya uraia kwa chama cha siasa, itakayokwenda kufanya programu yoyote ya kuwezesha kujengea uwezo vyama vya siasa lazima itoe taarifa kwa Msajili na ipeleke maudhui. Iwapo Msajili wa Vyama vya siasa ataona kwamba maudhui yaliyokusudiwa hayalindi utamaduni wetu, mila na desturi zetu, hailijengi Taifa letu katika umoja, amani na maendeleo yake atazuia na huo ndio wajibu wake. Kwa hiyo, hilo mimi naomba tusilipotoshe na Watanzania wote walijue. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni kupanua wigo wa Watanzania kushiriki katika masuala ya siasa bila kujali ukanda wala ukabila. Tunavyo vyama ambavyo ukivitazama vinatafsirika kama vyama vya ukanda, wakati mwingine vinatafsirika kama vyama vya kabila fulani. Sasa tukiendelea na utaratibu huu tutalimaliza Taifa letu, tutaliangamiza Taifa la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muswada huu umelitazama hilo, Ibara ya 13 ya muswada huu inamtaka yeyote anayesajili chama cha siasa, kwanza wanachama wapya wasipungue 200…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Spika alitahadharisha kuhusu muda mfupi tulionao. Kwa hiyo, taarifa na miongozo na kila kitu havitaruhusiwa isipokuwa utaratibu kama mtu anavunja kanuni.

Mheshimiwa Mhagama.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Katika kipengele hiki ambacho tunataka tulijenge Taifa lenye umoja, Taifa la Kitanzania, ambapo vyama vyote vya siasa viwe na uwiano sawa wa aina za wanachama waliopo katika vyama vyao ili Tanzania ibaki kuwa moja imetutaka Ibara ya 13 tuhakikishe kwamba wanachama wanatoka kwenye nusu ya mikoa ya Tanzania.

Vilevile pili imetutaka watoke walao kwa mikoa miwili ya Tanzania Zanzibar. Katika Tanzania Zanzibar walau Mkoa wa Pemba na Mkoa mmoja wa Zanzibar ya Unguja. Sasa tunataka nini Watanzania, tunataka kujenga Taifa moja na huu ndio uzuri mkubwa wa huu muswada na tusijikite kwenye vitu vidogo vidogo, tujikite kwenye mambo makubwa yanayokwenda kulijenga taifa la kujivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ambalo ningependa kuchangia ni kuimarisha utawala bora ndani ya vyama vya siasa. Moja katika tatizo tunalolipata sisi Watanzania tulijisahau. Usipojenga dhana ya utawala bora kwenye chama huwezi kuupata utawala bora kwenye Serikali, kwa sababu yeyote anayekwenda kulitumikia hili kama Waziri, atakayeshika nafasi ya urais, atakayeshika nafasi ya Uwaziri Mkuu, ametoka kwenye chama. Sasa tukiwa na chama ambacho hakina utawala bora utajenga Taifa gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunavyo vyaa ambavyo Mwenyekiti ndiye Accounting Officer, ndiye huyo huyo Afisa Masuuli, ndiye huyo huyo katibu, ndiyo msemaji wa chama. Sasa huyo huyo akipata nafasi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tutakuwa na taifa gani katika nchi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wito wangu ni kwamba, Watanzania tuuelewe muswada huu katika upana. Tusiende kwenye details ambazo hazina tija, tuangalie maudhui mapana ya taifa ambayo yanakwenda kulijenga Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno hayo naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.8) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 8). Kwa maslahi ya muda nitakwenda moja kwa moja kwenye hoja yangu, nataka kwanza nijikite kwenye hii Tasnia ya Maziwa, Sura ya 262.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya ajenda kubwa za Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali ya Jemedari Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ni kuhakikisha kwamba tunaifikisha Tanzania yetu kwenye uchumi unaotegemea viwanda. Moja katika maeneo makubwa ambayo yatachangia safari ya kuipata Tanzania ya viwanda ni sekta ya mifugo hususan eneo la maziwa na nyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya kuanzisha maabara ya maziwa, kifungu kipya cha 33A kinalenga kuipata Tanzania ya viwanda. Baadhi ya wadau wamechangia hapa hasa hotuba ya Kambi ya Upinzani wakati wanachangia ilionesha kuwa na maabara hii ni kama kupoteza rasilimali kwa sababu tuna maabara ya TBS. Ikumbukwe kwamba maabara ya TBS kazi yake ni kuangalia ubora na viwango katika ujumla wake, lakini tunapotaka kutengeneza bidhaa ambayo inataka kwenda kushindana kimataifa, tunataka kwenda kuuza kwenye ISO Standards ni lazima tuwe na maabara maalum ambazo zinajibu mahitaji ya masoko ya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, tayari tunazo maabara kama hizo hapa nchi, tuna maabara ya samaki ambayo inaitwa Water Quality Lab. Hii inalenga kuhakikisha kwamba samaki wanaovuliwa Tanzania kokote wanakokwenda kuuzwa ndani na nje ya nchi ubora wao kwa maana ya maji yaliyotumika unafahamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limefungua sana soko letu la samaki nje ya nchi, samaki wetu wameaminiwa nje ya nchi kwa sababu aina ya maji yanayotumika kuwakuza hao samaki inafahamika na imekubalika kimataifa. Tuna maabara za maji zipo mbili, ambazo nazo zinatumia ISO Standards, kwa maana hiyo maji yanayozalishwa kwa viwango hivyo yanaweza kuuzwa kokote dunia. Sisi Tanzania tunapotaka kwenda kwenye masoko ya kimataifa lazima bidhaa zetu zipate sifa hizo za viwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja katika zao ambalo litatupeleka katika masoko ya kimataifa ni zao hili la maziwa, kwa hiyo, niseme tu kwamba kwa Mheshimiwa Waziri kuleta marekebisho haya ameyaleta wakati muafaka kabisa na naomba Bunge lako tukufu liunge mkono kuanzisha maabara kwa kifungu cha 33A.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mfano wa maabara nyingine TFDA pamoja na majukumu mengine waliyonayo wana maabara ya food quality. Pamoja na TBS wapo lakini TFDA wana maabara, kwa hiyo, maabara hii isieleweke kwamba ni maabara mpya kabisa kwa maana ya kwamba hakuna practice hiyo nchini. Practice hiyo nchini ipo na inatusaidia kwenda kushindana kuzifanya bidhaa zetu zishindane kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili katika Sheria ya Tasnia ya Maziwa ni kuhusu Bodi ya Maziwa kifungu cha 9. Aina ya bodi iliyopendekezwa hapa ni Bodi ya Ushauri, Bodi hii ni tofauti na bodi ambayo ningesema ni executive. Ni bodi ambayo ina maamuzi na ni bodi ambayo inaweza kuchukua maamuzi. Bodi iliyopendekezwa hapa ni bodi ambayo kimsingi haiwezi kuchukua maamuzi zaidi ya kumshauri Mheshimiwa Waziri. Kwa vile tunataka kuijenga Tanzania ya viwango, kuipata Tanzania ya viwanda, naishauri Serikali kwanza ianzishe hii bodi, lakini bodi hii ibaki kuwa interim tu, tuendelee na mchakato sasa wa kuwa na bodi ambayo ni executive ambayo uteuzi wake utamhusu Mheshimiwa Rais na itakuwa na meno na itaweza kuisaidia sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama muda utaniruhusu naomba nichangie kidogo kwenye Sheria ya Chama cha Mawakili Tanganyika, Sura ya 307, kifungu cha 22 kinachoitaka tasnia hii mkutano mkuu ushiriki wake uzingatie uwakilishi. Chama cha Mawakili kinazidi kukua kwa idadi ya wanachama, kama kitaachwa hivi kilivyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naomba kuunga hoja mkono na ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2019
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru sana kwa kupata hii nafasi muhimu kuweza kuchangia Muswada huu uliopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu na kusema na iingie kwenye records kwamba naunga mkono Muswada huu ugeuke kuwa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niondoe upotoshaji mdogo unaoendelea wa kwamba tunashughulika na sheria 9. Muswada ni mmoja na unafanya marekebisho kwenye Sura 8. Natambua wadau wengi humu ni wanasheria, watalichukua hili kama maelezo sahihi, hakuna sheria 9, Muswada huu ni mmoja una Sura 8 na hizo ndizo tunazozifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niendelee kukupa comfort…

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Niendelee kukupa comfort kwamba…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mhagama, kuna taarifa, Mheshimiwa Salome.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kuwa Muswada huu unajadili mabadiliko ya sheria 9 ambazo ni Sheria ya Makampuni, Sura 212; Sheria ya Hakimiliki, Sura 218; Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza, Sura 230; Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Sura 56; Sheria ya Vyama vya Kijamii, Sura 333; Sheria ya Takwimu, Sura 351; Sheria ya Uwakala wa Meli, Sura 415 na Sheria ya Muunganisho wa Wadhamini, Sura 318. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mhagama, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nasikitika kwamba siwezi kuipokea hii taarifa…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Ni kwa sababu kama ambavyo yeye mwenyewe alishakiri kwamba Kamati imekaa weekend nzima kufanya kazi hii, ina uwezo wa kutofautisha katiya Sura 8 na sheria 9. Hatujadili sheria kamili, tunajadili Sura katika sheria hiyo. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya Watanzania naomba nitumie muda wangu uliobaki kuishauri Serikali. Moja nianze na kuipongeza kwamba tunazo principle tatu ambazo mimi ninazitumia katika maisha. Principle ya kwanza ni ku-focus, ya pili ni ku-sustain efforts na tatu ni ku-concentrate resources. Kama taifa tumejikita kwenye kuijenga Tanzania ya viwanda na ili tuijenge Tanzania ya viwanda tunahitaji kujenga mazingira bora ya makampuni yanayoshiriki katika kukuza biashara nchini. Makampuni haya tukiyaacha yamekaa holela holela kiasi ambacho hatuwezi kutofautisha kati ya kampuni ambayo ni guaranteed na shareholding, hatuwezi kuona namna gani tunaweza tukaratibu biashara nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa Sheria hii ya Makampuni, Sura ya 212 ambayo Serikali inapendekeza marekebisho yake naiunga mkono kwa asilimia 100 kwa sababu inaenda kuisaidia Serikali kwanza kujua walipa kodi ni wangapi kama makampuni. Kwa sababu tuna makampuni yamesajiliwa kama makampuni lakini yanafanya kazi yenye malengo yasiyo ya faida. Sasa kwenye makampuni kama hayo hatuwezi kwenda kuchukua kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ieleweke kwamba lengo la kuyaratibu haya, yale makampuni ambayo yanakwenda kufanya shughuli ambazo siyo za kifaida/ kibiashara yabadilishe utaratibu yakajisajili chini ya Sheria ya NGO, Na. 56 itakuwa ni utaratibu mzuri, sasa tutajua nani analipa na nani halipi kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitajikita kwenye maeneo ambayo pengine wajumbe waliotangulia hawakuyagusa. La pili, hii ajenda ya NGO kwa maana ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali imeleta kelele nyingi sana na pengine imepeleka message ovu ambayo Serikali haikukusudia kwa wadau. Kwanza, ieleweke kwamba Mashirika yasiyo ya Kiserikali nchini ni wadau muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu. Mashirika haya yanatusaidia kufanya tafiti mbalimbali, yanachangia Serikali, Halmashauri zetu za Wilaya, yanashirikiana na wakulima na maendeleo makubwa ambayo tumeyapata mpaka sasa huwezi kuondoa mchango wa taasisi zisizo za Kiserikali na hii Serikali inalijua. Kwa hiyo, wenzetu wasipeleke message tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mashirika haya ya Kiserikali yametusaidia sana katika masuala ya sera. Zipo sera nyingi ambazo zimefikiwa na zimekubaliwa ambazo zinaongoza shughuli mbalimbali za nchi yetu, zina mchango mkubwa sana wa wadau ambao ni NGOs. Kwa hiyo, mchango wa NGO nchi hii ni mkubwa sana na baadhi ya wadau humu ndani tusiwapotoshe wananchi na wala tusiyakatishe tamaa Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayofanya kazi nzuri sana katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii inalenga kuziratibu hizi NGOs, kuzijengea mazingira rahisi ya kufanya kazi ili pale ambapo wanakutana na vikwazo kama NGOs waweze kusaidiwa. Sasa imechukuliwa tu upande mmoja kana kwamba Serikali inataka izifute, hakuna mahali ambapo katika Miswada hii yote tuliyopita pamekusudia kuifuta NGO inayotekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili, nilikuwa tu na ushauri. Moja, tunayoyaona katika NGOs, kama nilivyosema zipo NGOs zinafanya kazi nzuri sana lakini zipo NGOs kama vichaka vya wala fedha za wafadhili. Sasa Serikali ina wajibu wa kuona kwamba fedha zinazoingia nchini kwa malengo ya kusaidia iwe utafiti, masuala ya sera, wananchi, wakulima wadogowadogo, kwenye maeneo ya elimu, vyuo vikuu ili mradi kwamba fedha hii ni ya wafadhili na inalenga kuboresha maeneo hayo, ifanye kazi zilizokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliokuwa huko mwanzo, ulikuwa ni kila mwaka NGO hizi zina-submit financial reports zikiwa audited. Utaratibu wa sasa umeboresha tu kwamba tusisubiri baada ya mwaka mzima, tuwe na quarterly reports ambazo zinaonesha kwamba nini kimefanyika katika kipindi hiki cha miezi mitatu, nani wamenufaika, wamenufaikaje, fedha kiasi gani kimetumika, kuna ubaya gani katika jambo hili? Ni utaratibu wa kawaida ni transparency. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tunazitaka Halmashauri zetu za Wilaya zifanye kazi kwa kuzingatia transparency, kama ambavyo tunaitaka Serikali Kuu ifanye kazi kwa transparency na vyombo vyote vingine vinavyoisadia Serikali zikiwemo NGOs lazima kuwe na transparency. Mimi ninaamini wadau wengi wanajua umuhimu wa transparency, hili halitawasumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu alipokuja kwenye Kamati alifafanua aina gani ya reports zinatakiwa kila miezi mitatu na kama wadau watapata nafasi na mashaka, watumie nafasi hii kujielimisha kupitia mamlaka husika zitatusaidia kuelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya muda nilikuwa na mchango mrefu kidogo lakini basi niishie hapo na naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na.3 wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kupata fursa ya kuchangia Muswada huu, na ni niungane na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kuchangia kwamba Muswada huu ni Muswada muhimu sana kwa Maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iingie kwenye kumbukumbu zako za Bunge kwamba Bunge lako limepitisha Miswada mingi sana muhimu kuwa Sheria ambayo imechangia sana ukuaji wa Uchumi wa Taifa letu. Lakini Muswada huu wa leo, Muswada wa marekebisho ya sheria mbalimbali namba tatu wa mwaka 2021 ni Muswada wa kipekee sana, kwa sababu unaenda ku-trigger kwa namna ya pekee sana ukuaji wa Uchumi wa Taifa letu, Muswada huu unaenda kufungua milango kwa uwekezaji mkubwa sana ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, limetajwa hapa Bomba la Mafuta huu ni moja tu, katika miradi mikubwa ambayo itakuwa accommodated na mabadiliko au na maboresho ya sheria hii. Mheshimiwa Rais akiwa Mwanza aliongelea mradi wa Liganga na Mchuchuma ambao unaenda kuzalisha chuma ya kutosha kwa Maendeleo ya Taifa letu, marekebisho ya sheria hii yana- accommodate miradi ya aina hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini juzi tu Mheshimiwa Rais ameongelea uwezekano na utayari wa Tanzania kukaa chini na wawekezaji kuona namna gani miradi ambayo ilisimama ianze, ikiwemo na mradi mkubwa wa bilioni 10 dola, dola bilioni 10 wa Bagamoyo, aina hii ya Miswaada inaenda ku-accommodate aina hiyo ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema utangulizi huo nitumie fursa hii kumpongeza sana sana Mhehimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia kuleta mabadiliko haya ya Sheria ili kuruhusu uwekezaji mkubwa na wenye maslahi makubwa kwa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iingie kwenye record za siku 100 za Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan za utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi haya mabadiliko ya kiuchumi yatakayotokana na mabadiliko ya sheria zilizopendekezwa yatakuwa ni ya kujivunia kwa kizazi hiki na kwa kizazi kijacho cha watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno hayo ya utangulizi nirudi kwenye muktadha wa sheria hii. Muktadha wa sheria hii wa mapendekezo haya unahusu miradi siyo mradi, inahusu miradi ambayo mikataba yake itakuwa na masharti maalum na itaridhiwa na Mabaraza la Mawaziri. Kwa hiyo, siyo mikataba bora mikataba ni mikataba yenye masharti maalum. Na nini kinapendekezwa na Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inapendekeza kwamba miradi hii ambayo ina masharti maalum ambayo pia itakuwa imeridhiwa na Baraza la Mawaziri vifungu vilivyotajwa hapa kwenye Sheria 14 visihusike utekelezaji wake, utekelezaji wa vifungu hivi vilivyotajwa hapa kwenye hizi sheria 14 utekelezaji wake usiathiri utekelezaji wa miradi au mikataba hii mikubwa iliyotajwa na hiyo ndiyo mantiki na hiyo ndiyo adhma ya mapendekezo haya ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa umuhimu wa miradi ya aina hii likiwemo pamoja na Bomba la Mafuta kutoka Hoima, naunga mkono kwa asilimia 100 mapendekezo yote yaliyoletwa na Serikali pamoja na marekebisho ya Kamati. Kwa vile muda unaniruhusu nataka nitaje maeneo matatu ambayo nadhani yanaweza kuchangia kuongeza uelewa wa Bunge lako Tukufu na Wabunge kuweza kupitisha sheria hii bila kuyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sehemu ya Tatu ya mapendekezo ya Sheria zinazopendekezwa inahusu Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura 191. Sheria hii ya Mazingira ilikuwa inazuia kufanyika shughuli zozote za kibinadamu ndani ya mita 60 ambako kuna vyanzo vya maji, mito, mabwawa na kadhalika. Sheria hii kama ingebaki hivi kwa miradi mikubwa, ikiwemo kama hii ya Bomba la Mafuta ingetukwamisha. Kwa hiyo, mabadiliko na mapendekezo haya ni muhimu sana ili kufanikisha mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hii Sehemu ya Sita, Sheria ya Bima, Sura ya 394. Pamoja na kifungu cha 133 kutaka mkazi yeyote wa Tanzania au makampuni yote ya Tanzania yanapotaka kupata huduma ya bima lazima yapate bima kwa kupitia makampuni ya Kitanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii ilikuwa inatukwamisha kwa sababu mradi huu pamoja na miradi ya aina hii ina masharti makubwa na ina gharama kubwa za bima, makampuni yetu ya ndani yanaweza yakakosa uwezo huo. Sheria hii inaruhusu kwa makampuni ambayo yatakuwa na sifa na masharti yaliyoelezwa hapa, tuweze kutumia hata bima za makampuni ambayo sio ya Kitanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maslahi ya muda, nakushukuru sana na naunga mkono hoja na naomba Watanzania na Wabunge wote tuunge mkono hoja hii ya Serikali. Ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2021
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kukupongeza wewe kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nature na Muswada huu, nitaomba niwe specific kwenye mchango wangu na nitajikita moja kwa moja kwenye Sehemu ya Nne ya Muswada unaopendekezwa. Sehemu ya Nne ya Muswada huu inafanya marekebisho ya Kifungu cha 91 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ambapo madhumuni ni kuzuia kukamatwa tena kwa mtuhumiwa ambaye ameachiwa huru kwa utaratibu wa nolle prosequi.

Mheshimiwa Spika, ili kuelewa vizuri haya mapendekezo ya Serikali, naomba nisome kifungu hicho cha 91 nikinukuu kwa sehemu. Kifungu cha 91 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Kifungu Kidogo cha Kwanza kinasema: “Katika kesi yoyote ya jinai na katika hatua yoyote ile, kabla ya hukumu au uamuzi, kama itakavyokuwa Mkurugenzi wa Mashtaka anaweza kuweka nolle prosequi, aidha, kwa kueleza Mahakama au kwa kuiambia Mahakama kuhusika kwa maandishi kwa niaba ya Jamhuri kuwa Mwenendo hautaendelea…”

Mheshimiwa Spika, ni ibara ndefu kidogo, lakini nitaenda kwenye hitimisho la Ibara hiyo ambapo anasema: “…lakini kuachiwa huko kwa Mtuhumiwa hakutachukuliwa kama kizuizi kwa mashtaka mengine ya baadaye dhidi yake na kwa kutumia maelekezo hayo hayo.”

Mheshimiwa Spika, practice imekuwaje? Kumekuwa na practice ambayo moja inaleta mzigo kwa Serikali, lakini pili, inaleta upendeleo. Katika mienendo ya kesi za namna hiyo, katika kutekeleza hicho kifungu cha 91 wapo watuhumiwa walioachiwa kwa utaratibu huo wa nolle prosequi, lakini utekelezaji wake siyo tu umeongeza mlundikano wa mahabusu Magerezani, lakini pia imeuletea mzigo mkubwa sana Serikali. Wengi wanaachiwa kwa utaratibu huu, lakini akishatoka tu getini, anakamatwa na anashtakiwa upya. Anaachiwa kwa utaratibu huu, anakamatwa anawekwa tena mahabusu. Kwa hiyo, utaratibu huu ni kama haujatusaidia kutatua tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia utekelezaji wa kifungu hiki cha 91, pamoja na kuwanufaisha Watanzania kwa baadhi, lakini wengi walionufaika ni watu wenye hadhi ya juu. Masikini wengi; watuhumiwa wengi ambao uchumi wao ni wa chini na hali yao ni ya chini, hawajanufaika vizuri na utaratibu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mapendekezo haya ya Serikali ambayo ningependa niyanukuu, yapo kwenye Ibara ya 25 ya Muswada na Fasili mpya ya (3). Naomba niyasome kama yalivyoandikwa:

“Where the accused is discharged under subsection one, he shall not be rearrested and charged on the same facts unless there is sufficient evidence and that the hearing of the case shall proceed immediately upon the rearrest of the accused person subject to section 131(a).”

Mheshimiwa Spika, ni kwa mara ya kwanza katika kipindi hiki kifupi cha Awamu ya Sita Serikali inaleta marekebisho ya Sheria ambayo ni very inclusive. Marekebisho haya yanaenda kuwafuta machozi Watanzania wengi; mamia kwa maelfu ambao wamewekwa Magerezani kwa muda mrefu, wameshitakiwa bila vielelezo na bila ushahidi. Kifungu hiki cha 131 (a) kinataka tusipeleke, tusikamate au kuwaweka watu vizuizini kabla hatujakamilisha ushahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vyombo vinavyohusika na ushahidi, vikamilishe Ushahidi. Mtu anapokamatwa, day two apandishwe kizimbani, ushahidi upelekwe, kesi iendeshwe na apewe haki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni la kipekee na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono Muswada huu kwa sababu unakwenda kutatua tatizo kubwa, siyo tu la mlundikano wa mahabusu magerezani au siyo tu gharama kubwa za uendeshaji wa Magereza yetu lakini unaenda kutoa haki kwa Watanzania wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naliomba tena Bunge lako kuunga mkono Muswada huu kwa maslahi mapana ya Watanzania hasa wanyonge.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 2) Act, 2022
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Muswada huu muhimu sana kwa maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niungane na Serikali pamoja na Kamati ya Katiba na Sheria kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia Serikali ilete muswada huu muhimu sana kwa maslahi ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Jaji Dkt. Eliezer Feleshi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa wasilisho lake zuri na kwa kushirikiana vizuri sana na Kamati ya Katiba na Sheria katika kuuboresha muswada huu.

Mheshimiwa Spika, kwa maslahi ya Watanzania na Waheshimiwa Wabunge naomba uniruhusu ninukuu taarifa ya Kamati katika Ibara ya 13 ya muswada. Taarifa ya Kamati inasema;

“Katika Ibara ya 13 Muswada unapendekeza kukifuta na kukiandika upya kifungu cha 32 cha sheria hiyo. Masharti mapya yanayopendekezwa yanawapa maafisa wa mamlaka madaraka ya kukamata, kupekua na kuchunguza makosa chini ya sheria hiyo.”

Mheshimiwa Spika, naomba pia uniruhusu ninukuu sehemu ya pili ya taarifa hiyo katika Ibara hiyo hiyo ya 13 inayozungumzia Ibara ya 32 ya Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Sura ya 95 ambayo inasema;
“Kifungu kipya cha 30 ambayo inaweka masharti katika kifungu kipya cha 32(4) na kifungu kipya cha 32(5) ambavyo kwa pamoja vinaipa mamlaka husika kwa maana ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya uwezo wa kuanzisha mahabusu zake na masharti ya kumuweka mtu kizuizini kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa katika sheria nyingine kabla ya mtuhumiwa kufikishwa mahakamani.”

Mheshimiwa Spika, Bunge lako litakubaliana na mimi kwamba madhara yanayotokana na matumizi ya dawa za kulevya ndani ya nchi yetu ni makubwa sana, vijana wengi wa Kitanzania ambao wameanguka kwenye matumizi ya dawa za kulevya wamekuwa vijana ambao Taifa haliwezi kuwategemea tena na wamekuwa mzigo mkubwa sana kwa Taifa. Nenda Zanzibar, lakini nenda Dar es Salaam, Mikoa mikubwa na midogo kokote utakakokwenda utakuta vijana wengi wameathirika na matumizi ya dawa za kulevya, lakini pia Serikali imebebeshwa mzigo mkubwa sana wa kuhudumia na kuwarudisha kwenye hali ya kawaida, hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Spika, pili, Bunge lako litakubaliana na mimi kwamba mtandao wa wauzaji wa dawa za kulevya ni mkubwa sana ndani ya nchi hii, pia unahusisha nchi za nje, kwa hiyo ni mtandao ambao ni complex sana kwa nature yake, siyo mtandao rahisi kuuvunja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, Bunge lako Tukufu litakubaliana na mimi kwamba kwa sehemu kubwa wanaojihusisha na kunufaika na biashara ya dawa za kulevya ni wafanyabiashara wakubwa sana, matajiri wakubwa ndani na nje ya nchi yetu. Kwa hiyo, siyo watu wadogo ambao tunaweza kukabiliana nao kirahisi.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu pia litakubaliana na mimi kwamba njia ambazo zinatumika kusafirisha dawa za kulevya ni ngumu na ni njia ambazo kimsingi zinahitaji utaalam maalum wa kuweza kukabiliana nazo. Nitatoa mfano. Unajua kwamba baadhi ya dawa za kulevya zinasafirishwa kwenye tumbo la binadamu, wanaosafirisha wanameza kete zinakaa tumboni kwa saa nyingi, 48 au zaidi. Na hiyo ni moja kati ya njia ngumu ambazo zinatumika kusafirisha dawa za kulevya. Pia zinasafirishwa kwa njia za meli, njia za boti, kupitia wavuvi kwenye bahari bubu. Kwa hiyo, hizo hoja nne zinadhihirisha kwamba kupambana na biashara ya dawa za kulevya kunahitaji umahsusi, umakini, utaalam, ujuzi wa kipekee na zaidi kunahitaji nyenzo za kipekee sana.

Mheshimiwa Spika, hali ilivyo sasa, kulitegemea Jeshi la Polisi peke yake kukabiliana na tatizo hili tunafeli. Sayansi, takwimu zimethibitisha kwamba tunafeli kwa kiwango kikubwa sana. Usambazaji wa dawa za kulevya na uingizaji wake umeendelea kuwa mkubwa ndani ya nchi yetu licha ya Jeshi la Polisi kuwepo.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo ambayo yametolewa na Mamlaka hii ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ni kwamba sasa wapate mamlaka kamili ya kuweza kukabiliana na jambo hili huku wakisaidiana na Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, yapo mazingira ambayo tumeona, mtu ambaye ameshikwa na dawa za kulevya anapelekwa kwenye custody hizi mnasema rumande, anawekwa ndani, anatafutiwa ushahidi, kabla ushahidi haujakamilika ushahidi mtaani umepotea kwa sababu kuna interaction kubwa sana kati ya Jeshi letu la Polisi, watu wengine ambao wanakaa ndani nao lakini pia wale ambao wanashiriki kwenye huo mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mapendekezo ya Serikali ni kwamba tuwe na mahabusu maalum ambazo zitatumika kukabiliana na tatizo hili ili yule ambaye amekutwa na dawa za kulevya achukuliwe awekwe kwenye mahabusu maalum ili pia tupate fursa ya kulinda ushahidi ambao upo mtaani ambao mara nyingi umekuwa unapotea kwa sababu watu hawa wakiachiwa au wakiwa na interaction na watu wengine ambao wamekosa uadilifu au watu wengine ambao wapo kwenye mahabusu ambao hawana kesi kama hizo basi ushahidi huo unapotea na tunashindwa kulimaliza tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikubaliane na pendekezo la Serikali kuunga mkono hoja hii kwamba Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ipewe sasa kibali cha kuwa na mahabusu yao waweze kupambana na jambo hili kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwanza kukushukuru wewe mwenyewe kwa kutupa nafasi ya kuchangia Bungeni. Lakini kipekee sana nikushukuru kwa niaba ya Kamati yetu ya Utawala, Katiba na Sheria kwa kutupa jukumu hili kwa niaba ya Waheshimiwa Wabunge ili tupate nafasi ya kulitazama, kulichambua na kuishauri Serikali, tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuishukuru Sekretarieti yako ambayo ulitupa kwa kweli wametupa ushirikiano mkubwa sana na matokeo ya kazi hii ambayo umeiona mezani kwako ni mapato ya mchango mkubwa wa Sekretarieti yako pia.

Mheshimiwa Spika, nilitamani pia mbele ya Bunge lako hili Tukufu niwashukuru sana sana Waheshimiwa Mawaziri ambao walibeba Miswada hii na kuilete mbele ya Kamati yako. Kwanza Mheshimiwa George Boniface Simbachawene (Mb) Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora lakini Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro (Mb), Waziri wa Katiba na Sheria pamoja na Manaibu Waziri, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete na Mheshimiwa Gekul kwa kweli wametupa ushirikiano mkubwa sana kama Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitakuwa na fadhila kama sitamshukuru Mwanasheria Mkuu, Dkt. Feleshi ambaye amekuwa na Kamati katika kipindi chote cha kuchambua na kujadili. Tumekuwa tunajibizana mpaka kwa WhatsApp kwa hoja mbalimbali. Kwa kweli Serikali ilijipanga vizuri na imetoa ushirikiano mkubwa sana kwa Kamati yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeona kwenye taarifa yetu ya Kamati, takriban asilimia 90 ya maoni, mapendekezo na ushauri wa Kamati, Serikali imechukua. Kwa kweli unaona hii ni Serikali ya aina gani, ni Serikali sikivu, ni Serikali iliyokubali kwamba nje ya Serikali kuna mawazo mazuri na kuna mawazo chanya yanayoweza kulijenga Taiafa letu. Kwa hiyo, nilitamani sana niweke hii kumbukumbu ya kudumu mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu ni Serikali sikivu haiji na mambo yake Bungeni ila inakuja na maoni na inapokea na maoni ya wadau na Wabunge kama ambavyo umeshuhudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu uchambuzi wa maeneo mbalimbali, Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia wamechangia kwa kikamilifu sana; na ninaamini wamelisaidia sana Bunge lako Tukufu kuelewa misingi ya mabadiliko yalioletwa na misingi ya sheria mbalimbali ambazo zimeletwa; lakini kubwa zaidi maeneo ambayo yanenda kuleta tija sana kwa maendeleo ya Taifa letu. Ninashindwa ku-comment vifungu vingi kwa sababu kwa sehemu kubwa Waheshimiwa Wabunge wamevitaja. Lakini kwa sababu tu ya msisitizo nitaje maeneo machache ambayo nadhani ni muhimu Waheshimiwa Wabunge wakarudia kuyasikiliza.

Mheshimiwa Spika, moja katika changamoto ambazo tulikua nazo ni kuwa na mipango mizuri lakini mipango isiyolindwa na sheria. Kwa hiyo, tumekuwa na mipango, tunapanga kila mwaka, tunarudia kwenye bajeti, Liganga na Mchuchuma inazungumzwa miaka 30 lakini hakuna hatua inayochukuliwa kwenye utekelezaji wake. Liganga na Mchuchuma ni moja katika miradi mikubwa ya kielelezo ya Taifa letu lakini hakukua na namna ya kuilinda kisheria. Sheria hii ya Tume ya Mipango imekuja na Kifungu Ibara ya Sita; na Mheshimiwa Dkt. Alice amesema, Mheshimiwa Mwinyi amesema na Makamu Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Katiba na Sheria, Mheshimiwa Florent Kyombo amesema; kwamba imelindwa sasa.

Mheshimiwa Spika, katika Ibara ya 6 inasema mpango wowote, Ibara ya 6(4) na hii, naomba nirudie, hii imekuja kama Schudule of Amendment, imekuja kama jedwali la marekebisho baada ya Kamati kuishauri Serikali ilinde mipango hii ambayo tunaiweka. Serikali niwashukuru sana mlipokea maoni haya ya Kamati mkaenda kutafuta namna gani mipango yetu tuilinde, na hiyo ndiyo namna pekee ambayo tutaisimamia mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali imekuja na marekebisho ya jedwali, jedwali la marekebisho Schedule of Amendment Ibara ya 6(4), inasomeka kama ifuatavyo: “Mpango wowote wa muda mfupi au wa muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa sheria hii au sheria nyingine iliyotungwa na Bunge na kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara ya 63(3)(c) ya Katiba hautabadilishwa au kuachwa kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge”. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni moja katika ibara muhimu sana katika Sheria ya Tume ya Mipango kwa sababu nchi hii mipango tunayo, nchi hii mawazo mazuri tunayo lakini hatuyalindi na hatuyalindi kwa sheria. Kwa hiyo moja katika maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge walitaja; na nitambue mchango mzuri wa Askofu Gwajima na Waheshimiwa Wabunge ambao walichangia eneo hili kwamba tuulinde. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili kwa maslahi ya muda naona kengele ya kwanza imegonga. Ibara ya 20 inayofanya marekebisho Kifungu cha 19 cha sheria kuhusu suala la good faith; na nimuombe Mheshimiwa Makamba. Good faith imetafsiriwa kwenye sheria, naomba nimwachie hiyo assignment kwenda kutafuta tafsiri hiyo, lakini wanansheria hapa mpo mnajua good faith imetafsiriwa na hili ni suala la Kimahakama upon convinction kwamba umekutwa na hatia. Kwa hiyo, hili jambo lipo kisheria, niliomba nimuongoze mdau mwenzetu na mdau wetu mzuri sana wa masuala ya sheria, Mheshimiwa Makamba kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nilitaka pia kama muda utaruhusu, Ibara ya 5(e) inaongelea ulinzi wa Presidential Candidate during the general election ambapo kulikuwa na intervention kutoka kwa Mheshimiwa Waziri ambayo ni very relevant intervention, inahusu ulinzi wa wagombea nafasi ya Urais. Sasa kwa sehemu Mheshimiwa Waziri amesema lakini kwa sehemu naomba niseme na hii pia naomba nimu-address Mheshimiwa Salome Makamba.

Mheshimiwa Spika, tunapoongelea ulinzi ambao unatolewa na Idara ya Usalama wa Taifa ni tofauti na aina ya ulinzi unaotolewa na vyombo vingine vya ulinzi na usalama. Kazi ya Usalama wa Taifa, Idara ya Usalama wa Taifa imeelezwa kwenye Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa, sheria mama, Kifungu 5 (1) (a) mpaka (d) zinaeleza majukumu ya Idara ya Usalama wa Taifa. Kwa hiyo, aina ya ulinzi tunaouzungumza sio hu ambao wenzetu wa Dar; na nilimsikia Mheshimiwa Zitto Kabwe kwenye mijadala huko nje akizungumza. Naomba arejee kwenye ibara hii inayoweka wigo wa shughuli za Idara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la muhimu zaidi, arejee pia kwenye Muswada uliopendekezwa. Muswada uliopendekezwa ibara hiyo hiyo ya 5A wamefafanua kazi za Idara ya Usalama wa Taifa. Kwa hiyo tunapoongelea aina ya ulinzi kwa viongozi, haiondoi vyombo vingine vya ulinzi na usalama kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mambo mengi ya kuzungumzia, yamesemwa mengi lakini nitumie nafasi hii kukushukuru sana na niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono hoja yetu ya Kamati. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwanza kukushukuru wewe mwenyewe kwa kutupa nafasi ya kuchangia Bungeni. Lakini kipekee sana nikushukuru kwa niaba ya Kamati yetu ya Utawala, Katiba na Sheria kwa kutupa jukumu hili kwa niaba ya Waheshimiwa Wabunge ili tupate nafasi ya kulitazama, kulichambua na kuishauri Serikali, tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tuishukuru Sekretarieti yako ambayo ulitupa kwa kweli wametupa ushirikiano mkubwa sana na matokeo ya kazi hii ambayo umeiona mezani kwako ni mapato ya mchango mkubwa wa Sekretarieti yako pia.

Mheshimiwa Spika, nilitamani pia mbele ya Bunge lako hili Tukufu niwashukuru sana sana Waheshimiwa Mawaziri ambao walibeba Miswada hii na kuilete mbele ya Kamati yako. Kwanza Mheshimiwa George Boniface Simbachawene (Mb) Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora lakini Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro (Mb), Waziri wa Katiba na Sheria pamoja na Manaibu Waziri, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete na Mheshimiwa Gekul kwa kweli wametupa ushirikiano mkubwa sana kama Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitakuwa na fadhila kama sitamshukuru Mwanasheria Mkuu, Dkt. Feleshi ambaye amekuwa na Kamati katika kipindi chote cha kuchambua na kujadili. Tumekuwa tunajibizana mpaka kwa WhatsApp kwa hoja mbalimbali. Kwa kweli Serikali ilijipanga vizuri na imetoa ushirikiano mkubwa sana kwa Kamati yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeona kwenye taarifa yetu ya Kamati, takriban asilimia 90 ya maoni, mapendekezo na ushauri wa Kamati, Serikali imechukua. Kwa kweli unaona hii ni Serikali ya aina gani, ni Serikali sikivu, ni Serikali iliyokubali kwamba nje ya Serikali kuna mawazo mazuri na kuna mawazo chanya yanayoweza kulijenga Taiafa letu. Kwa hiyo, nilitamani sana niweke hii kumbukumbu ya kudumu mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu ni Serikali sikivu haiji na mambo yake Bungeni ila inakuja na maoni na inapokea na maoni ya wadau na Wabunge kama ambavyo umeshuhudia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu uchambuzi wa maeneo mbalimbali, Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia wamechangia kwa kikamilifu sana; na ninaamini wamelisaidia sana Bunge lako Tukufu kuelewa misingi ya mabadiliko yalioletwa na misingi ya sheria mbalimbali ambazo zimeletwa; lakini kubwa zaidi maeneo ambayo yanenda kuleta tija sana kwa maendeleo ya Taifa letu. Ninashindwa ku-comment vifungu vingi kwa sababu kwa sehemu kubwa Waheshimiwa Wabunge wamevitaja. Lakini kwa sababu tu ya msisitizo nitaje maeneo machache ambayo nadhani ni muhimu Waheshimiwa Wabunge wakarudia kuyasikiliza.

Mheshimiwa Spika, moja katika changamoto ambazo tulikua nazo ni kuwa na mipango mizuri lakini mipango isiyolindwa na sheria. Kwa hiyo, tumekuwa na mipango, tunapanga kila mwaka, tunarudia kwenye bajeti, Liganga na Mchuchuma inazungumzwa miaka 30 lakini hakuna hatua inayochukuliwa kwenye utekelezaji wake. Liganga na Mchuchuma ni moja katika miradi mikubwa ya kielelezo ya Taifa letu lakini hakukua na namna ya kuilinda kisheria. Sheria hii ya Tume ya Mipango imekuja na Kifungu Ibara ya Sita; na Mheshimiwa Dkt. Alice amesema, Mheshimiwa Mwinyi amesema na Makamu Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Katiba na Sheria, Mheshimiwa Florent Kyombo amesema; kwamba imelindwa sasa.

Mheshimiwa Spika, katika Ibara ya 6 inasema mpango wowote, Ibara ya 6(4) na hii, naomba nirudie, hii imekuja kama Schudule of Amendment, imekuja kama jedwali la marekebisho baada ya Kamati kuishauri Serikali ilinde mipango hii ambayo tunaiweka. Serikali niwashukuru sana mlipokea maoni haya ya Kamati mkaenda kutafuta namna gani mipango yetu tuilinde, na hiyo ndiyo namna pekee ambayo tutaisimamia mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali imekuja na marekebisho ya jedwali, jedwali la marekebisho Schedule of Amendment Ibara ya 6(4), inasomeka kama ifuatavyo: “Mpango wowote wa muda mfupi au wa muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa sheria hii au sheria nyingine iliyotungwa na Bunge na kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara ya 63(3)(c) ya Katiba hautabadilishwa au kuachwa kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge”. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni moja katika ibara muhimu sana katika Sheria ya Tume ya Mipango kwa sababu nchi hii mipango tunayo, nchi hii mawazo mazuri tunayo lakini hatuyalindi na hatuyalindi kwa sheria. Kwa hiyo moja katika maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge walitaja; na nitambue mchango mzuri wa Askofu Gwajima na Waheshimiwa Wabunge ambao walichangia eneo hili kwamba tuulinde. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili kwa maslahi ya muda naona kengele ya kwanza imegonga. Ibara ya 20 inayofanya marekebisho Kifungu cha 19 cha sheria kuhusu suala la good faith; na nimuombe Mheshimiwa Makamba. Good faith imetafsiriwa kwenye sheria, naomba nimwachie hiyo assignment kwenda kutafuta tafsiri hiyo, lakini wanansheria hapa mpo mnajua good faith imetafsiriwa na hili ni suala la Kimahakama upon convinction kwamba umekutwa na hatia. Kwa hiyo, hili jambo lipo kisheria, niliomba nimuongoze mdau mwenzetu na mdau wetu mzuri sana wa masuala ya sheria, Mheshimiwa Makamba kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nilitaka pia kama muda utaruhusu, Ibara ya 5(e) inaongelea ulinzi wa Presidential Candidate during the general election ambapo kulikuwa na intervention kutoka kwa Mheshimiwa Waziri ambayo ni very relevant intervention, inahusu ulinzi wa wagombea nafasi ya Urais. Sasa kwa sehemu Mheshimiwa Waziri amesema lakini kwa sehemu naomba niseme na hii pia naomba nimu-address Mheshimiwa Salome Makamba.

Mheshimiwa Spika, tunapoongelea ulinzi ambao unatolewa na Idara ya Usalama wa Taifa ni tofauti na aina ya ulinzi unaotolewa na vyombo vingine vya ulinzi na usalama. Kazi ya Usalama wa Taifa, Idara ya Usalama wa Taifa imeelezwa kwenye Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa, sheria mama, Kifungu 5 (1) (a) mpaka (d) zinaeleza majukumu ya Idara ya Usalama wa Taifa. Kwa hiyo, aina ya ulinzi tunaouzungumza sio hu ambao wenzetu wa Dar; na nilimsikia Mheshimiwa Zitto Kabwe kwenye mijadala huko nje akizungumza. Naomba arejee kwenye ibara hii inayoweka wigo wa shughuli za Idara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la muhimu zaidi, arejee pia kwenye Muswada uliopendekezwa. Muswada uliopendekezwa ibara hiyo hiyo ya 5A wamefafanua kazi za Idara ya Usalama wa Taifa. Kwa hiyo tunapoongelea aina ya ulinzi kwa viongozi, haiondoi vyombo vingine vya ulinzi na usalama kutekeleza majukumu yake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mambo mengi ya kuzungumzia, yamesemwa mengi lakini nitumie nafasi hii kukushukuru sana na niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono hoja yetu ya Kamati. (Makofi)