Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Vicky Paschal Kamata (1 total)

MHE. VICKY P. KAMATA aliuliza:-
Kampuni kubwa za uchimbaji madini kama vile GGM, Buzwagi Gold Mine na North Mara Gold Mine licha ya kulipa kodi kwa Serikali kuu pia zinawajibika kuhudumia jamii inayozunguka migodi kwa utaratibu wa uwajibikaji kwa jamii kwa kutoa fedha au kufadhili miradi ya kijamii au maendeleo:-
• Je, kwa mwaka 2017 Kampuni hizo kila moja ilitoa fedha kiasi gani?
• Je, hadi kufikia Januari mwaka 2018, Kampuni hizo zimetoa kiasi gani.
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Vicky Kamata, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 105(1) na (2) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017, kinamtaka mmiliki wa leseni kuandaa mpango wa mwaka wa utaratibu wa uwajibikaji kwa jamii (corporate social responsibility). Mpango huo lazima ukubalike kwa pamoja na Mamlaka ya Serikali ya Mtaa husika kwa kushauriana na Halmashauri ulipo mgodi kwa kuzingatia vipaumbele vya Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya mpango huo yanapaswa kumshirikisha Waziri wa Fedha na Mipango, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kabla ya kuidhinishwa na Baraza la Madiwani la Halmashauri husika. Aidha, kila Halmashauri ulipo mgodi inapaswa kuandaa mwongozo wa uwajibikaji kwa jamii kwenye Halmashauri yao, kusimamia utekelezaji wake na kutoa elimu kwa wananchi wa Wilaya husika juu ya huduma hizo.
Mheshimiwa Spika, kwa takwimu zilizopo, migodi ya Geita Gold Mine, Buzwagi Gold Mine na North Mara Gold Mine imekuwa inatekeleza jukumu hili la kutoa huduma za jamii zinazozunguka migodi hiyo. Huduma ambazo zimekuwa zinatolewa ni kwa maeneo ya afya, elimu, maji, mazingira, ujasiriamali, miundombinu na jamii kama vile barabara, majengo na masuala ya sanaa na utamaduni.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2017, mgodi wa North Mara ulitumia dola za Marekani 1,837,495, sawa na takribani shilingi bilioni 4.25 kwenye huduma za jamii. Mgodi wa Buzwagi ulitumia dola za Kimarekani 595,658.47, sawa na shilingi bilioni 1.38 na mgodi wa Geita Gold Mine, dola za Kimarekani 6,358,542.24 sawa na shilingi bilioni 14.45.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kumekuwa na changamoto za gharama halisi za miradi hiyo. Kunaonekana ziko juu sana ukilinganisha na gharama halisi ya kile kilichotekelezwa. Marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017 yaliyofanyika yanataka sasa Halmashauri zihusishwe katika kufanya maamuzi kuhusiana na mipango ya uwajibikaji kwa jamii.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018, migodi hiyo mitatu imekwishaandaa mpango kazi wa utekelezaji wa uwajibikaji kwa jamii. Maandalizi ya mpango yameshirikisha Serikali za Mitaa kama sheria inayowataka na kuwasilishwa kwa Halmashauri husika kwa ajili ya utekelezaji. Hadi kufikia Juni, 2018 mgodi wa Geita Gold Mine unatarajiwa kutumia kiasi cha dola za Kimarekani 1,932,142 na mgodi wa North Mara jumla ya dola za Kimarekani 333,111.39 na mgodi wa Buzwagi jumla ya Dola za Kimarekani 224,215.24