Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Fatma Hassan Toufiq (41 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Na mimi naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuweza kusimama katika hili Bunge Tukufu kuzungumzia kuhusu hotuba ya Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuzungumza ndani ya Bunge hili, naomba nichukue fursa hii kuwashukuru sana wanawake wa Mkoa wa Dodoma kwa kunichagua na kunifanya niwe Mbunge wao. Sambamba na hilo niwashukuru pia wanaume wa Mkoa wa Dodoma kwa kuwaruhusu wake zao na watoto wao kuweza kuja kunichagua kwa hiyo, nawashukuru sana wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kwa unyenyekevu mkubwa kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri aliyoitoa. Nalipongeza pia Baraza la Mawaziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana kuzungumzia kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukurasa wa 73 ambao ulikuwa unazungumzia suala la Ustawishaji Makao Makuu. Naamini sote tunafahamu kwamba suala la Ustawishaji wa Makao Makuu lilianzishwa mwaka 1973 lakini kwa masikitiko makubwa sana mpaka leo hii hakuna sheria ambayo inazungumzia uwepo wa Makao Makuu Dodoma. Kukosekana kwa sheria hiyo imechelewesha sana kuhamia Makao Makuu Dodoma. Pamoja na taarifa nzuri ambayo imetolewa kwamba kuna baadhi ya mambo yamepangwa katika Ustawishaji Makao Makuu, lakini kumbe ipo sababu ya msingi kabisa ya kutungwa sheria ambayo itaharakisha Makao Makuu yawe Dodoma na Ofisi ziweze kuhamia Dodoma, hatimaye Mji Mkuu wa Tanzania yetu uwe Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, labda niwakumbushe tu kwamba wenzetu Nigeria walibaini kwamba wanatamani wapate Mji Mkuu mpya mwaka 1976, wakajitahidi by mwaka 1991 wakaweza kufanikiwa kuhama kutoka Lagos kwenda Abuja. Sisi tangu mwaka 1973 mpaka leo mwaka 2016 bado hatujaweza kuhamia Dodoma. Kwa kweli hili jambo inabidi zichukuliwe hatua za uhakika kuhakikisha kwamba sheria hii inatugwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo wa sheria ya kutambua kwamba Dodoma ni Makao Makuu utasaidia sana kwa sababu kuna muingiliano mkubwa sana wa utendaji kati ya Manispaa pamoja na hii Mamlaka ya Makao Makuu. Kwa hiyo, naamini kwamba ukiwekwa mkazo wa uhakika kutungwa kwa hii sheria utasaidia kabisa kutofautisha kazi kati ya Manispaa pamoja na hii Mamlaka ya Ustawishaji wa Makao Makuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo ni kwamba uwepo wa sheria ile utasaidia kuharakisha kuwa na uwekezaji katika Mkoa wetu wa Dodoma. Kwa kweli katika Mkoa wa Dodoma, miaka ya nyuma kulikuwa na baadhi ya viwanda kwa mfano, Kiwanda cha Coca-cola lakini tunashangaa kiliondoka vipi, kulikuwa kuna Kiwanda cha Mvinyo bahati mbaya kikafa, kulikuwa kuna Kiwanda cha Magodoro, tunaona tu Magorodo Dodoma lakini magodoro yale hayatengenezwi hapa Dodoma.
Kwa hiyo, naamini kabisa kama ukiwekwa mkazo na naamini katika Bunge hili tutahakikisha sheria hii inatungwa basi uwekezaji utaweza kupata tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ili kupunguza mwingiliano wa kazi kati ya Manispaa pamoja na CDA, ikiwezekana kiundwe chombo kimoja tu ambacho kitasimamia ustawi na upimaji wa mipango miji katika Mkoa wa Dodoma kwa sababu Manispaa wanafanya shughuli hizohizo ambazo zinafanywa na CDA. Kama sheria itaweka chombo kimoja ambacho kitasaidia sasa kufanya mambo yote ya mipango miji, naamini kabisa itasaidia ustawishaji na hatimaye Makao Makuu yanaweza yakaja Dodoma lakini kubwa zaidi ni suala la sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie pia suala la miundombinu. Katika Mkoa wetu wa Dodoma pamoja na kwamba mji umepangwa vizuri lakini kuna maeneo tofauti tofauti kwa mfano maeneo ya Area C, Nkuhungu, Medeli na maeneo mengine mapya ambayo yameanza kujengwa, zile barabara za ndani za mitaa hazipo, mvua zikinyesha kwa kweli kunakuwa na adha kubwa sana kwa wananchi. Kuna maeneo ambapo mashimo ni makubwa sana, kuna maeneo mifereji iliyopo sio mifereji ambayo inaweza ikasaidia kupitisha maji, kwa hiyo inaleta madhara makubwa sana. Kwa kuwa Waziri Mkuu yupo hapa na analisikia sheria hii ikitiliwa mkazo naamini kabisa mambo mengi yanaweza yakafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kulisisitiza ni kuhusu sewage system katika huu Mkoa wa Dodoma. Kuna maeneo ni kweli imejengwa sewage system, lakini maeneo mapya ambayo Ustawishaji Makao Makuu wameyaweka sewage system bado sio nzuri. Kwa hiyo, tunaomba na jambo hilo lifikiriwe kwa ajili ya afya ya wananchi wa Mkoa wa Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nililokuwa nataka nilizungumzie ni kuhusu uwanja wetu wa ndege katika eneo la Msalato. Ninaamini kabisa kwamba uwanja huu uko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini bado sijaona hatua za haraka au zinazoenyesha kwamba uwanja huu unaweza kujengwa haraka. Kwa sababu uwanja huu kwa kweli utakuwa una tija sana kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma lakini pia na wananchi wengine wote wa Tanzania kwa ujumla. Kwa hiyo, nimeona na hilo nalo nilizungumzie ili uwanja huo nao uweze kuangaliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni kwamba katika Mkoa wa Dodoma kuna eneo karibu kama kilometa nane kutoka pale Chuo cha Mipango bado halijawekwa lami. Kwa kweli imekuwa ni kero sana kwa wananchi na wamekuwa wakiilalamikia sana Serikali kwa kuona ukimya uliopo kwa sababu limekuwa la muda mrefu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naamini kabisa katika bajeti hii nalo litatiliwa mkazo ili kusudi eneo lile liweze kuwekewa lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia ni kuhusu suala la maafa na majanga na hasa kwenye janga la moto. Tumekuwa tukisikia matukio mbalimbali kuhusu janga la moto lakini bado nchi yetu haina vifaa vya kutosha kwa ajili ya kukabiliana na janga hili. Kwa hiyo, niombe Serikali waone ni utaratibu gani tunaoweza kuufanya walau wa kuweza kupata magari na vifaa vya uokozi wa moto katika kila Wilaya ili kusudi inapotokea dharura yoyote ya moto waweze kupata fursa ya kuweza kuzima huo moto kwa sababu wananchi wengi sana wamekuwa wakipata hasara.
Mheshimiwa Naibu Spika, mengi wameyazungumza wenzangu kuhusu masuala ya afya, maliasili na kadhalika lakini naomba tu nizungumzie kidogo kuhusu suala la Bima ya Afya au CHF. Wenzangu wamelizungumza na mimi naomba nitoe msisitizo, hebu Serikali ione kwa sababu hii asilimia 27 ya wachangiaji ni asilimia ndogo sana, bado tuna sababu ya msingi sana ya kuhamasisha wananchi ili kusudi waweze kujiunga na huu Mfuko wa CHF kwa sababu una tija sana kwao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo la kushangaza sana Watanzania wenzangu hatuko makini sana kuchangia masuala mbalimbali ya kimaendeleo. Watu wako makini sana kuchangia harusi na sherehe mbalimbali, lakini kwenye suala afya inaonekana watu hawana mwamko. Nitoe shime kwamba na sisi viongozi tulifanyie kazi suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hii hoja iliyopo mbele yetu lakini pia sambamba na hilo naomba nichukue fursa kuungana na wenzangu wote kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango, Naibu Waziri Dkt. Ashatu, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii. Ndugu zangu pamoja na maneno yote naomba muendelee kuchapa kazi kwa sababu kazi mnayoifanya inaonekana. Naomba niwatie shime kwa hilo kwa hiyo msikate tamaa maisha ni mapambano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia ukurasa wa 31 hadi ukurasa wa 33 wa hotuba hii mmezungumzia kuhusu vipaumbele ambavyo vimewekwa. Naomba nipongeze sana Serikali na Wizara kwa ujumla kwa kuweka vipaumbele hivi na hasa kwenye suala zima la vipaumbele vya kilimo na viwanda. Juhudi zinaonekana pamoja na ufinyu wa bajeti lakini Serikali inajitahidi sana. Niipongeze tena Serikali kwa kuwa na hii program ya kuendeleza kilimo ya ASDP II. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo nina ushauri, kwamba Serikali imejipanga kujaribu kuona jinsi gani pembejeo zinaweza zikapatikana na kadhalika, lakini bado naomba nisisitize suala la wataalam. Kwa kweli suala la wataalam bado wataalam hawatoshelezi, huku katika maeneo ya kata na vijiji ambako ndiyo wako wakulima zaidi kwa kweli wataalam hawako wa kutosha. Kwa hiyo utakuta kwamba wanalima mazao bila kufuata zile taratibu za kitaalam, kwa hiyo, nilikuwa niiombe Serikali yangu tukufu waone umuhimu sasa wa kuona jinsi gani wataalam zaidi wanaweza kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo wataalam hawa inabidi waandaliwe kuanzia katika shule za msingi ili watoto waone kwamba kilimo ni sehemu ya ajira na wasione kwamba kilimo ni adhabu. Kwa hiyo, kama wakitengenezwa kuanzia katika ngazi ya chini, naamini kabisa tutaweza kupata watalaam wengi zaidi. Ni ukweli usiopingika kwamba, kwa kuwa Tanzania yetu inakwenda kwenye uchumi wa viwanda suala la malighafi lazima lipatikane, na hizi malighafi lazima zipatikane humuhumu nchini ili kusudi wananchi wetu na wakulima wetu waweze kupata tija. Kwa hiyo, bado niendelee kushauri kwamba upo umuhimu kabisa wa kuhakikisha kwamba bajeti ya kutosha inapangwa hasa kuhakikisha kwamba wataalam wanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuhimiza mapinduzi ya viwanda lakini bado tunategemea kilimo cha mvua, na wenzangu wengi wamelizungumza hili kwamba hakika itabidi lazima tufanye mkakati wa uhakika wa kuhakikisha kwamba kilimo kinakuwa ni kilimo cha umwagiliaji badala ya kilimo cha mvua. Tumeona hivi karibuni jinsi gani mvua ambavyo zimechelewa na jinsi gani mazao yalivyoathirika, kwa hiyo, nitoe shime kwamba tuone kwamba suala la kilimo cha umwagiliaji kipewe kipaumbele ili kusudi sasa tuweze kupata zile malighafi kwa ajili ya kulisha hivyo viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la uendelezaji wa suala la zao la zabibu. Niendelee kuipongeza Serikali suala zima la kupunguza ile bei ya mchuzi wa zabibu lakini bado ilikuwa ili kuliongezea hili zao la zabibu thamani isiwe ni mvinyo tu, lakini zipatikana bidhaa nyingine zinazotokana na zabibu mfano juice, pengine jam na mazao mengine ambayo yatatokana kutokana na hii zabibu. Kwa hiyo, tuhamasishe uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo na hasa kwa wanawake ili kusudi waweze kutengeneza hizi bidhaa mbalimbali ambazo zinatokana na zabibu na ikiwezekana wapewe fursa ya kutengeneza mchuzi wa zabibu hatimaye waweze kuuza katika hivi viwanda vikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, zabibu hizi zinaweza zikakaushwa. Zikikaushwa zabibu naamini kabisa zitaleta sana tija kwa nchi yetu hasa Mkoa wa Dodoma kwa wakazi na wakulima wa Mkoa wa Dodoma. Kwa sababu zabibu kavu nazo zina soko zuri sana na zabibu hizi zinaweza zikailetea pato Taifa letu. Kwa sababu inaonekana kabisa kwamba zabibu hizi nyingi hazitengenezwi hapa instead zinaagizwa kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, zabibu za kukausha basi Serikali ione tunawezaje kupata mitambo ya kutosha ili kusudi sasa wananchi wetu waweze kukausha hizi zabibu na hatimaye Serikali yetu iweze kupata pato la kutosha. Sambamba na hilo, suala zima la zabibu za mezani. Zabibu ambazo zilizopo kwa mfano katika Mkoa wa Dodoma bado zabibu za mezani hazijaweza kupatiwa pembejeo za kutosha. Kwa hiyo, basi nione kwamba Serikali nayo ione kwamba kwenye hili suala la zabibu za mezani nazo ziweze kupatikana ili kusudi tuepuke kuagiza kutoka nje tuweze kuongeza pato letu la ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusiana na Benki ya Kilimo, naipongeza sana Serikali kwa kuanzisha benki hii. Hata hivyo, bado nitoe shime kwamba benki hii iongezewe mtaji na Serikali ili kusudi wananchi wengi zaidi waweze kufaidika na hii Benki ya Kilimo mwisho wa siku wananchi waweze kupata tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilikuwa nataka nizungumzie Serikali ione utaratibu wa kuweza kuweka reserve ya maji ili maji haya yaweze kutumika kipindi cha kiangazi hasa katika kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie kuhusu vifungashio au mifuko ambayo inatumika kwa ajili ya kuweka mazao. Kuna ile mifuko ya kawaida lakini kuna ile mifuko ambayo mazao yakiwekwa mazao yale yanaweza yakakaa kwa muda mrefu sana. Kwa hiyo, nilikuwa naomba niitie shime Serikali kwa sababu wakulima wengi sana kwanza hawana taarifa kuhusu hii mifuko ambayo ni bora zaidi lakini sambamba na hilo mifuko hii ni bei ghali sana kwamba mfuko mmoja unafika mpaka shilingi 5,000. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali ione umuhimu sasa au wa kupunguza VAT, au wa kuona jinsi gani mifuko hii inapunguziwa bei ili mwisho wa siku wakulima wote waweze kupata tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie kuhusuana na suala la taulo za kike, taulo za kike kwa sababu wenzangu wengi sana wamelizungumzia na hii iko katika ukurasa wa 38. Pamoja na Serikali kutoa ule msamaha wa kodi ile ya VAT, nilikuwa naomba niishauri Serikali hebu kuona ni jinsi gani kama ikiwezekana tuweze kuweka bei elekezi, bei ambayo itakuwa ni affordable. Kwamba kila mtu au kila mtoto wa kike anaweza akai-afford hiyo taulo ya kike, lakini sambamba na hilo kwa kuwa kuna vifaa ambavyo vinatumika kwa ajili ya kutengeneza hizi pad, basi ufanyike utaratibu wa kutengeneza reusable pads. Nakumbuka wakati ule sisi tunasoma tulikuwa tunafundishwa jinsi ya kutengeneza reusable pads ili kusudi watoto hawa waweze kuzitumia. Kwa hili suala la reusable pads pia linawezekana ili kusudi watoto waweze kuwa na taulo kwa wakati wote bila matatizo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kwamba naomba nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali kwa kutoa ile miezi sita ya uanzishaji biashara, kwamba ile grace period. Kwa kweli hii Serikali imefanya jambo zuri sana kwani hii itasaidia sana wafanyabiashara na itasaidia baadhi ya wafanyabiashara kuanzisha biashara zao na hivyo kufanya suala la kukwepa kodi likapungua. Kwa hiyo, lakini naomba nitoe rai kwa wakadiriaji hili Mheshimiwa Mpango pamoja na kuandika kwenye hotuba yako basi hawa wakadiriaji pia wawe fair sana wasiwe wanafanya kwa ajili ya kukomoa wafanyabiashara. Kwa sababu mfanyabiashara pamoja na Serikali ni marafiki na huo urafiki inabidi lazima uendelee kwa sababu tunategemeana wote, mfanyabiashara pamoja na Serikali. Serikali inategemea kodi ya mfanyabiashara na mfanyabiashara nae anategemea Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nipongeze pia suala la dawati la malalamiko la ukadiriaji wa kodi. Niipongeze sana Serikali kwa jambo hili kwa sababu hii itasaidia sasa wafanyabiashara wengi kwenda kutoa malalamiko yako na hatimaye kuweza kupatiwa ufumbuzi. Nishukuru sana kwa kunipa fursa, naomba niendelee kuiunga mkono hoja. Ahsante sana, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza Wizara ya Elimu kudahili Walimu tarajali 5,690 katika vyuo vya UDOM, Kleruu na Monduli. Pamoja na kudahili wanafunzi hao inaonyesha kuna upungufu wa Walimu 22,000 wa sayansi bado tuna hitaji kubwa sana la kudahili Walimu zaidi. Wizara ingefikiria kufanya programu maalum walau miaka nane (8) ili kuzalisha Walimu wa Sayansi nchini kwa wingi kwa kuwapeleka vyuo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, naipongeza Serikali ya Awamu ya Nne kwa kujenga maabara katika kila sekondari za kata. Naipongeza pia Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuweka bajeti ya kununua vifaa kwa ajili ya maabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, inaonekana pia kuna upungufu wa Walimu wa lugha hasa Kiingereza. Je, kwa nini Wizara isirejee utaratibu wa miaka ya themanini hadi miaka ya tisini ambapo Walimu walikuwa wanasoma kwa michepuo? Kwa mfano:-
(i) Marangu – Kiingereza
(ii) Korogwe – Kiswahili
(iii) Mkwawa – Sayansi
(iv) Monduli – Kilimo
(v) Mandaka/Monduli - Kilimo
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa michepuo ulidahili wanachuo kutokana na ufaulu wao. Je, kwa nini Wizara isirejee mtindo huu ili kupata Walimu waliosomea masoma hayo? Wizara iangalie wapi tulikosea?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Waziri kuna mradi wa Education and Skills for Productive Jobs Programme (ESPT). Mradi una nia ya kukuza stadi za kazi na ujuzi. Sekta zilizopo ni sita (6) nazo ni za kukuza uchumi, kilimo, uchumi, utalii, uchukuzi, ujenzi, nishati na TEHAMA. Nashauri fani ya ushonaji na upishi nazo ziongezwe. Wizara inaweza kuona fani hii si hitaji lakini fani ya ushonaji/upishi ni fani ambazo zimeinua wananchi wengi katika ujasiliamali. Inabidi wanafunzi waanze kufundishwa fani hizi tangu msingi ili kuwaandaa wakifika VETA waweze kupata ujuzi mzuri zaidi na itasaidia vijana wengi kujiajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu maalum wengi wameizungumzia. Nashauri Wizara ifanye utaratibu wa kufanya sensa ya watoto wenye ulemavu kwani watoto wengi wenye ulemavu wanafichwa. Katika ukurasa wa 97, kiambatanisho (6) kinaonesha idadi ya wanachuo wenye ulemavu wanaodahiliwa katika vyuo ni kidogo sana. Tunataka kujenga Taifa lenye uchumi wa kati ni budi Serikali ikaona umuhimu wa kudahili wanachuo wengi zaidi wenye ulemavu ili nao waweze kupata fursa nyingi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sula la maslahi ya Walimu TSD ambayo sasa ni TSC inabidi ipewe nguvu ya kufanya kazi. Ni vema Wizara ya Elimu na TAMISEMI kuona jinsi ya kuipatia fedha za kutosha ili Walimu waweze kuhudumiwa vizuri zaidi. Kwa kuwa TSC inasimamia Walimu wa shule ya msingi/sekondari katika masuala ya nidhamu, maadili, kupandisha vyeo, kuthibitisha Walimu kazini na kutoa vibali vya kustaafu, vikao vya kisheria (statutory meetings) havifanyiki kutokana na ukosefu wa fedha. Inabidi Wizara ya Elimu na TAMISEMI waiangalie TSC kwa jicho la pekee ili waweze kutekeleza majukumu yao vizuri kwa ajili ya ustawi wa Walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wadhibiti Ubora wa shule za msingi/sekondari, ukurasa wa 18. Naipongeza Serikali kwa kusomesha Wadhibiti Ubora 1,435 ambao wamepata mafunzo ya stadi za KKK ili kutoa msaada kwa Walimu wanaofundisha KKK. Pamoja na kuwepo kwa Wadhibiti hao ni vema Wizara ikaweka utaratibu maalum wa kuwapeleka masomoni Walimu kipindi cha likizo ili wapate mafunzo rejea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 10, kipengele cha 5.0, mapitio ya utekelezaji wa majukumu kwa mwaka 2015/16, katika kusimamia utekelezaji na mambo yaliyobainishwa nazungumzia kipengele (v), naomba pia Walimu wa michezo wapewe mafunzo ili waweze kuwafundisha watoto wetu michezo kwani hakuna ubishi michezo ni ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza tena Wizara ya Elimu, Waziri na timu yote. Nawatia moyo waendelee na kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Naibu Waziri na Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote wa Wizara kwa kuandaa hotuba hii. Kwa kuwa nilichangia kwa kuongea kuna baadhi ya masuala ambayo sikuweza kuongea kutokana na muda. Naomba kuyachangia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na NGO nyingi zinazofanya kazi zinazofanana katika eneo moja, hii huwachanganya wakulima kutokana na duplication ya kazi. Aidha, kuna baadhi ya wakulima wanaamini NGO zipo kwa ajili ya kufuja fedha. Mfano, kuna NGO zinafanya kazi eneo la Iringa Vijijini, ni budi Serikali ikawapa ushauri NGO’s wafanye mipango kwanza ili kujua NGO ipi inafanya kazi katika eneo lipi? Aidha, NGOs zinapoenda kuomba kibali cha kufanya kazi ni budi Halmashauri wakatoa ushauri, yale maeneo yaliyofikiwa na NGO yasipelekewe huduma na NGO hizo badala yake wawape maeneo mapya katika kutekeleza miradi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Extension Officers wapo wachache, hawana msemaji wa fani, kwani wakipelekwa katika maeneo ya Vijiji/Ward/Wilaya hawapati mafunzo ya mara kwa mara yanayoendana na teknolojia ya kisasa. Aidha, ukosefu wa vitendea kazi ni kikwazo kikubwa katika utekelezaji majukumu ya Mabibi Shamba na Mabwana Shamba. Vifaa mfano magari, pikipiki na ukosefu wa mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wadudu waharibifu hasa katika Kanda ya Kati, ndege waharibifu aina ya Kwelea Kwelea. Nashauri Serikali ifanye utaratibu wa kununua ndege yake ya kunyunyuzia dawa ili pindi inapotokea ndege waharibifu dawa ziweze kunyunyiziwa kwa muda sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Idara ya Mifugo ukurasa wa 106 wa hotuba umebainisha kupungua kwa uzalishaji wa maziwa. Nashauri Serikali ibaini maeneo na kugawa mashamba kwa wafugaji na wapate utaalam wa kupanda majani kwa ajili ya chakula cha mifugo. Aidha, ni budi Serikali ikapata idadi kamili ya wananchi ambao ni wafugaji wadogo wadogo nchini ili kubaini nao wanazalisha maziwa kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado suala la unywaji maziwa shuleni upo katika kiwango kidogo, ni budi wadau mbalimbali wakashirikishwa ili waweze kusaidia suala la utoaji maziwa kwa watoto shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia bajeti hii. Sambamba na hilo naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema, nimpongeze sana Waziri wa Fedha kwa hotuba yake yote aliyoitoa ya Hali ya Uchumi pamoja na hotuba ya Bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite kwanza kwenye pato la ukuaji wa uchumi lakini nikirejea ukurasa wa 16 wa Taarifa ya Hali ya Uchumi. Naipongeza sana Serikali kwa kuifanya nchi yetu Pato la Taifa likakua kwa asilimia 7.0 kwa mwaka 2015. Nitoe masikitiko yangu kwamba kwenye eneo la kilimo ambapo asilimia 70 ya wananchi wetu ndiyo wanakitegemea imebainika kwamba uzalishaji wake umeshuka. Mwaka 2014 ilikuwa na asilimia 3.4 mwaka 2015 imeshuka kwa asilimia 2.1. Jambo hili hatutakiwi kulifumbia macho na halitakiwi tu kubakia katika vitabu. Tujiulize anguko hili limetokea kwa sababu ya nini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana wakulima wetu wamekata tamaa ama kwa kucheleweshewa pembejeo, pembejeo hazifiki kwa wakati lakini sambamba na hilo ni kwamba Vyama vyetu vya Msingi na Vyama vya Ushirika, vimekuwa vikidhulumu sana wakulima wetu. Kwa hiyo inawezekana kabisa Wakulima hawa wamekata tamaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inasababau ya makusudi sana kwamba nchi yetu tufikie kipato cha kati, lakini naomba niishauri Wizara, tukitegemea mvua za masika kwa kweli hatutafika. Ipo sababu ya msingi kabisa Serikali ikaona umuhimu wa kuweka kipaumbele katika kilimo cha umwagiliaji kwa sababu tukitegemea tu mvua za msimu mwisho wa siku tutakuja kukwama, kwa sababu tunaona kuna kipindi mvua za msimu zinakuwa ni nyingi sana, kuna kipindi zinakuwa ni chache. Ningeomba niishauri Serikali iweke mkakati wa muda mrefu wa kuhifadhi maji ya mvua ili mwisho wa siku tuweze kukajikite zaidi kwenye kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni budi sasa nchi yetu ikajitahidi kupata wataalamu wengi zaidi na kujifunza kutoka maeneo mbalimbali duniani kwa wenzetu ambao wameweza kufanikiwa katika kilimo cha umwagiliaji. Kwa mfano; wenzetu wa Israel wamefikia hatua nzuri, wenzetu wa Indonesia, wenzetu wa China na maeneo mengine duniani ambayo sikuyabainisha. Hebu Serikali yetu ifanye dhamira ya dhati kwa kuwapeleka wataalam wengi zaidi ili kusudi na sisi tuweze kujikita katika hili suala la kilimo cha umwagiliaji. Mwaka huu katika kilimo kumekuwa kuna shida sana hasa kwenye maeneo yale ambayo yanayolima mtama, maeneo ambayo yana uhaba wa mvua. Ni kwamba kumekuwa na ndege wengi sana ambao wamekuwa wakiharibu mazao, lakini kwa masikitiko makubwa sana, nchi yetu haina ndege ya kuweza kunyunyiza dawa. Ninaunga mkono mpango wa Serikali wa kununua ndege kwa ajili ya abiria, lakini hebu tuone kwamba je, kwa nini Serikali isifikirie zaidi kwa kununua ndege ambayo itasaidia kunyunyiza dawa kwenye yale maeneo ambayo watakuwa wanahitaji? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea zaidi kujikita kwenye suala la kilimo. Tumeona kwamba kwenye bajeti ya kilimo ni asilimia 4.9 ya bajeti, lakini bajeti hii bado ilikuwa haijafikia hata nusu ya lile Azimio la Maputo la mwaka 2003. Je, tujiulize, hivi ni kweli kabisa tunavyosema kwamba tunataka tufikie hatua ya kati na tunategemea mali ghafi kutoka kwa wakulima, kwa asilimia 4.9 ya bajeti yote, kweli tutafikia hilo lengo? Mimi naomba Serikali ione kwamba hili jambo inabidi tujipange upya kuhakikisha kwamba angalau bajeti ya kilimo nayo inafikia zaidi ya nusu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwenye pembejeo hasa matrekta, kulikuwa na matrekta ambayo yalitolewa kwa wananchi wakakopeshwa. Labda tu mimi nipate ufahamu, yale matrekta yaliyokopeshwa, wale wananchi waliokopa, je, wamerudisha kwa utaratibu mzuri? Je, ni muendelezo gani ambao unafanyika kuwe kuna revolving kwamba wale ambao waliokopeshwa yale matrekta wanayarudisha na wananchi wengine zaidi wanafaidika kupata yale matrekta. Isiwe utaratibu kwamba watu wakiona kwa sababu matrekta haya ni ya Serikali basi mtu akichukua halipi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kufahamishwa pia, je ni wananchi wangapi ambao pia wameendelea kufaidika baada ya wale wa mwanzo kuchukua mkopo huo? (Makofi)
Naomba pia nizungumzie suala la mifugo. Inasemekana kwamba miongoni mwa nchi ambazo zina mifugo mingi Tanzania pia ni mojawapo, lakini bado sekta ya mifugo haijaleta tija sana kwenye Pato la Taifa. Kwa hiyo naomba niishauri Wizara na nimshauri Waziri kwamba hebu katika bajeti kwa ajili ya ujenzi wa majosho, majosho kwa kweli bado yako katika hali mbaya sana, pamoja na dawa kwa ajili ya mifugo kwa sababu kama kweli tunasema kwamba tunataka tuanzishe viwanda vya kusindika na viwanda hivyo ni pamoja na viwanda vya nyama, sasa kama tukiwa na mifugo ambayo hali yake ni dhoofu kweli hivyo vya kusindika tutaweza kuvipata? (Makofi)
Naomba nishauri kwamba hebu tuone kwamba lazima suala la majosho liangaliwe upya lakini pia kuna baadhi ya yale mashamba ambayo yalitelekezwa kabisa, mashamba ya mifugo. Mashamba yale yamevamiwa na wananchi na mengine yameachwa zaidi ya miaka 22. Hebu tuone Serikali iwe na nia ya dhati ya kufufua mashamba yale ili kusudi sasa kama kweli tunataka kupata hivyo viwanda vya kusindika tuweze kuvipata.
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi wamezungumzia sana kuhusu suala la afya na mimi pia naomba nizungumze. Katika bajeti yetu, Wizara ya Afya imetengewa asilimia 9.2 ambayo vilevile haijafikia lile Azimio letu la Abuja, Serikali ivute soksi kuhakikisha kwamba angalau tunafikia asilimia ile ili kuboresha afya za wananchi wetu. Kwa kweli inabidi Serikali ijipange zaidi, kwani tunapozungmzia afya, kama mtu asipokuwa na afya bora maana yake elimu haitakuwa bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim M. Majaliwa, kuhusu hatuba ya Bajeti aliyoiwasilisha Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika kipindi cha mwaka mmoja wa Uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mengi yamefanyika. Nampongeza sana juhudi zinazofanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza juhudi zinazofanywa na Mheshimiwa Rais kuhakikisha Serikali inahamia Dodoma. Bado napenda kukumbusha sheria ya kuhamia Dodoma haijapitishwa katika Bunge lako Tukufu. Je nini kinasababisha ucheleweshaji wa utungaji wa Sheria
hii. Pamoja na nia nzuri ya Serikali kuhakikisha Dodoma inakuwa Makao Makuu, kumekuwa na malalamiko ya baadhi ya wananchi katika maeneo mbalimbali mfano Nkuhungu Centre, Kiwanja. P. 639 wanalalamika pamoja na kulipia viwanja vyao lakini wengine wamenyang’anywa kwa madai wameshindwa kuviendeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linaweza kuleta mgogoro mkubwa sana kati ya Serikali na wananchi, hata kama kuna baadhi ya wananchi wameshindwa kuendeleza maeneo ni vema wakapewa taarifa ili ithibitike mapema isiwe Serikali inapokea pesa ya kodi na baadhi ya wananchi
wanazo slip za Bank ambazo wamekuwa wanazilipia kodi zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kuwa Serikali hii ni sikivu ni vema kufuatilia kwa ukaribu jambo hili ili kupata ukweli. Pia Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu hayo inatakiwa itende haki kwa wale wote waliovamia maeneo, hali kadhalika Kamati za Makazi nazo zifuatiliwe kwani kuna baadhi ya Wanakamati hao wanafanya udanganyifu wa kuuza maeneo bila kufuata utaratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza Serikali suala la ukusanyaji mapato unaofanywa na TRA, lakini mamlaka inabidi itumie mbinu mbadala ili ulipaji kodi uwe hiyari na wananchi waone ulipaji kodi ni wajibu wa kila Mtanzania. Kwani mtindo unaotumika wa kutumia maaskari na mabunduki mengi inaleta hofu. Ushauri wangu elimu ya mlipa kodi au ulipaji kodi ni kwa ajili ya maendeleo ya nchi katika masuala yote ya kijamii, elimu, afya, miundombinu, kilimo na ufugaji ni kwa maendeleo ya Watanzania wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuweka dhamira ya dhati katika kuendeleza kilimo cha biashara, pamoja na kuzalisha mbegu za nafaka ni budi pia kilimo cha biashara cha mbogamboga ambacho kimeanza kuwa na tija na kikitiliwa mkazo kitasaidia kupunguza
umaskini kwani kilimo cha mbogamboga mfano matikiti maji, matango, carrots, hoho, vitunguu, nyanya na mboga zingine zinaweza kuongeza pato la Taifa, iwapo Taifa litaweka mkazo na kufanya tafiti zaidi na kuzalisha mbegu za mbogamboga. Ili zizalishwe kwa wingi, kwa bei nafuu ili ikiwezekana mazao ya mbogamboga yaweze kuzalishwa kwa wingi na hatimaye kusafirisha nchi mbalimbali duniani. Kwani uhitaji wa mazao ya mbogamboga ni mkubwa sana na una tija kwa wazalishaji mazao hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ukame na njaa, pamoja na wadudu waharibifu nalo ni jambo la kuliangalia kwa jicho tofauti. Kutegemea mvua katika kilimo bado kunasababisha njaa, kwani mvua hazitoshelezi kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo ni budi Serikali ijikita katika kilimo cha umwagiliaji na pia uvunaji maji ya mvua ili yatumike kumwagilia kipindi cha kiangazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya maeneo ikiwemo kanda ya Kati, Mikoa ya Dodoma na Singida, pia baadhi ya mikoa inayolima mazao ya mtama, mfano Shinyanga kumekuwa na tatizo la ndege waharibifu ushauri wangu Serikali ifanye utaratibu wa kupata ndege yake ili inapotokea uharibifu wa ndege iwe rahisi kutekelezwa kwa haraka kuliko kusubiri ndege ya kutoka Nairobi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa vita dhidi ya rushwa na madawa ya kulevya. Bado mkazo utiliwe na Serikali kutoa elimu kwa jamii waone ubaya wa rushwa, pia kwa vijana kujihusisha na madawa ya kulevya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kujenga uchumi na viwanda na kuimarisha viwanda vyetu bado naendelea kushauri, wananchi wa Tanzania wahamasishwe kuzalisha malighafi kwa ajili ya kuhudumia viwanda. Kwani tukiwa na viwanda halafu malighafi ikaletwa kutoka nje haitakuwa na maana. Ni budi Serikali ikaweka mkakati wa makusudi ili kuhakikisha malighafi zaidi zinazalishwa nchini ili ziweze kukidhi mahitaji ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza ujenzi wa miundombinu vijijini unaotekelezwa na kampuni ya Viettel, je, ni ofisi ngapi za Wakuu wa Wilaya zimepatiwa miundombinu ya mitandao ya Internet nauliza jambo hili kwa sababu baadhi ya Ofisi za Wakuu wa Wilaya hazina huduma
za Internet. Nahitimisha kwa kumpongeza tena Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami nichangie hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote kwa kuandaa bajeti hii ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye biashara ya uwindaji. Inabidi ikumbukwe kwamba biashara hii ni biashara tofauti sana na biashara nyingine. Uwindaji wa kitalii ni shughuli ambayo ni starehe kwa watalii husika, hivyo basi ni dhahiri kwamba Watalii hawa wanapokuwa wamekuja kwa ajili ya uwindaji wa kitalii wanahitaji kuwa na mazingira ambayo yametunzwa vizuri na yako vema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna tishio kubwa sana la uvamizi wa mifugo katika mapori yetu mbalimbali au mapori ya akiba na hii imekuwa ni kikwazo sana kwa uwindaji wa kitalii na hata hii imesababisha asilimia 34 ya uwindaji wa kitalii ukaporomoka kati ya 2013 na 2017. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aone kwamba hii tunapoteza pato la Taifa, kwa hiyo ipo sababu ya msingi kabisa kwa Serikali kuona inafanya mkakati wa kuhakikisha kwamba mifugo haikai katika haya mapori ya akiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirejee kwamba kupoteza hii asilimia 34 ya vitalu kwa kweli Taifa linakosa mapato makubwa sana. Kwa mfano, Serikali inakosa mapato kwenye ile daraja la kwanza kabisa la vitalu US$ 60,000, hii ni pesa ya kutosha sana. Sambamba na hilo kwenye grade ya pili tunakosa US$ 30,000 na kadhalika na kadhalika mpaka grade ya tano ni US$ 5,000. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla ione kwamba kweli hapa Serikali inakosa mapato kwa sababu tu ya mifugo kuingia katika mapori haya. Naomba nitoe shime kwamba lazima uwepo mkakati wa uhakika wa kuhakikisha kwamba mifugo haiingii katika mapori haya.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nibainishe kwamba kwa kuwa sekta ya utalii inaingiza asilimia 25 ya fedha za kigeni na kuchangia asilimia 17 ya pato la Taifa, hivyo naendelea kusisitiza kwamba ni budi Serikali ikawa na mkakati endelevu wa kuhakikisha kwamba tunaweza kupata pato zaidi kwa kuboresha miundombinu iliyopo katika maeneo yote ya hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nizungumzie sekta hiyo ya utalii hasa nishauri kwamba, sekta ya mifugo pamoja na Halmashauri zijitahidi sana kusimamia Sera ya Mifugo kwa kutenga maeneo ili kusudi wafugaji waweze kupata maeneo yao waweze kuweka mifugo yao kule. Hii pengine inaweza ikasaidia mifugo isiingie katika hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ni budi tuwe na takwimu sahihi za mifugo iliyopo katika nchi hii na kila mfugaji abainike kwamba ana mifugo mingapi. Pia wafugaji lazima wahamasishwe tu wafuge kwa tija ili mwisho wa siku Serikali iweze kupata mapato kwa kutokana na utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nizungumzie suala la misitu katika mabonde na mito. Haina shaka kwamba tatizo la uharibifu wa mazingira binadamu ndiyo wahusika wakuu. Kwa hiyo, maeneo mengi sana yameharibiwa, maeneo mengi sana yamekatwa miti na kadhalika hasa kwenye maeneo ya mabonde. Nashauri kwamba, Serikali pia ije na mkakati wa nguvu wa kuhakikisha kwamba maeneo yale ambayo ni ya mabonde yahifadhiwe na yapandwe miti mingi sana kwa sababu ile mito na maziwa ambayo yanakauka inatokana na ukataji miti, hivyo nilikuwa nashauri Serikali ilisimamie hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba nisisitize tena suala la upandaji wa miti ili tuweze kukilinda kizazi hiki na kizazi kijacho, watoto wetu na wajukuu zetu na vitukuu wasije wakatulaumu kwamba sisi tulishindwa, kwa hiyo suala la udhibiti wa mazingira ni lazima lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba pia nichangie idara ya utalii ya mambo ya kale. Kuna mwenzangu mmoja ameshalizungumzia hili lakini nami naomba niongezee. Ili Taifa liweze kupata kipato ni budi Serikali yetu iendelee kutangaza vivutio vya utalii pamoja na malikale. Kwa mfano, katika maeneo ya fukwe, mapango, kuna miongoni mwetu ambao pia wamezungumzia kuhusu suala la mila na desturi za makabila mbalimbali, historia za viongozi, pamoja na mila za makabila na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, hapa kwetu Mkoani Dodoma Wilaya ya Kondoa kuna mapango ambayo michoro yake iko katika historia ya dunia. Je, Serikali imetangaza kiasi gani Wilaya hii ya Kondoa ili kusudi nayo iwe ni mojawapo ya kivutio cha watalii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Afrika ya Kusini, kuna utalii wa mila na desturi ambao unaendelezwa kule, sisi tuna zaidi ya makabila 120. Je, tumejiandaaje makabila haya nayo yaweze kuwa kivutio cha watalii? Tuna makabila mbalimbali, tuna Wamasai, tuna Wayao, tuna Wanyakyusa na mengine ambayo sikuyataja, wote hawa wana mila zao na desturi, hebu nasi tuone ni kwamba tunafanyaje kuhusu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba pia niishauri Serikali ifanye utaratibu wa kutuma wataalam wetu katika maeneo mbalimbali ya Afrika na nje ya Afrika, kuona wenzetu wamewezaje kufanikiwa katika hili suala zima la utalii. Sisi tuna vivutio vingi sana sana duniani, lakini bado hatujaweza kuwavutia watalii kiasi hicho. Nashauri Serikali ingefanya utaratibu wa kuwapeleka wataalam mbalimbali ili kusudi waje walete ujuzi kutoka maeneo hayo angalau na sisi itusaidie kupaisha sekta yetu ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nichukue fursa hii kushukuru sana na kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuleta sera ya elimu bure, sambamba na hilo naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Elimu kwa bajeti hii ambayo imeletwa mbele yetu ambayo leo hii tunaizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina baadhi ya masuala ambayo ningependa kuyachangia na iwapo kama muda utaniruhusu basi nitaendelea zaidi, lakini katika mambo ambayo ningependa kuyachangia ni pamoja na udhibiti wa elimu, suala la upatikanaji wa vitabu shuleni ambalo wengi wetu wamegelizungumzia, sambamba na hilo ni uanzishwaji wa bodi ya kitaalam ya walimu, suala la programu ya lipa kulingana na matokeo pamoja na elimu ya kujitambua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 85 amezungumzia kuhusu kuboresha mazingira ya elimu kwa wadhibiti ubora wa elimu. Kwanza niipongeze sana Serikali kwa kuamua kwamba watajenga ofisi 50 kwa ajili ya udhibiti wa elimu. Pamoja na pongezi hizo bado kuna changamoto nyingi sana na naamini kabisa Mheshimiwa Waziri analitambua hilo hasa kwenye ofisi zetu za udhibiti wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi natokea Mkoa wa Dodoma, tuchukulie ofisi yetu ya Udhibiti wa Elimu Kanda ya Kati. Kwa kweli baadhi ya vifaa hakuna, suala zima la samani, vitendea kazi na kadhalika. Hali kadhalika magari hayatoshelezi, sasa hapa tunazungumzia kuhusu kuboresha elimu, bila kuwa na vifaa vya kutosha je, tutafikia hili lengo kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niishauri Wizara hebu haya ambayo tunayazungumza hapa wayafanyie kazi, pamoja na kwamba katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba watanunua kompyuta 100, lakini sambamba na hilo kwamba kuna baadhi ya Wilaya mpya ambazo zimeanzishwa, mimi naona idadi hii bado ni kidogo ni budi Wizara ikaongeza vifaa vingi zaidi kwa ajili ya utendea kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwamba ofisi nyingi za Udhibiti wa Elimu ni za kupangisha, kumekuwa na changamoto kubwa sana kwa sababu kwanza ya ucheleweshaji wa OC, wale watendaji wanaokaa katika ofisi hizi kwa kweli wamekuwa wakipata taabu sana na karaha kwa sababu OC imekuwa ikichelewa pengine miezi sita mpaka miaka miwili, kwa hiyo hii kwa kweli inawaletea karaha sana. Ninaishauri Wizara ni vizuri sasa ikaweka mkakati wa uhakika wa kupeleka OC kwa muda unaotakiwa ili kusudi watu hawa wasipate karaha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kuna hili suala la elimu bure ambapo kwenye sera ya elimu bure inatakiwa kwamba kila mwanafunzi wa sekondari katika ile capitation fee inatakiwa shilingi 1,000 ipelekwe kwenye Idara ya Ukaguzi au Udhibiti wa Shule. Kwa masikitiko makubwa naomba niseme kwamba pesa hizi mara nyingine huwa hazifiki na hivyo kuchelewesha kabisa utendaji wa udhibiti elimu. Ninatoa ushauri kwa Mheshimiwa Waziri kwamba pesa hizi zimekuwa zikikatwa, lakini zikikatwa zimekuwa zikipelekwa katika akaunti ya Wizara na baadaye ndiyo zinakuja kupelekwa kwenye akaunti za Kanda. Hebu waone ili kupunguza urasimu ni vizuri kwamba pesa hizi zikikatwa zipelekwe moja kwa moja kwenye Ofisi za Kanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia suala la upatikanaji vitabu pia na udhaifu. Wenzangu wengi sana wamelizungumzia na hapa nina kitabu cha Steps in Primary Mathematics Book Four for Tanzania. Kitabu hiki kimetungwa na Mtunzi ambaye anaitwa Kireri K.K.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu kina maajabu sana, maajabu yake ni kwamba hapa nina vya huyu mtu mmoja ambaye amevitunga Ndugu Kireri K. K. Katika vitabu hivi ukweli ni kwamba yaliyoandikwa humu huwezi ukaamini, naomba jamani kwanza nilikuwa najiuliza hivi kweli EMAC ipo? Kwa sababu kuna baadhi ya vitabu vina ithibati ya EMAC, lakini kuna vitabu vingine havina ithibati ya EMAC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ina maana kwamba hapa kuna issue ya pirating, tuone Wizara ifanye utaratibu wa kwenda katika kila shule na kufanya ukaguzi wa kujua kwamba vile vitabu halali ni vipi na visivyo halali ni vipi. Nina-declare interest mimi ni mwalimu by profession na nimekuwa Afisa Elimu Vifaa na Takwimu kwa zaidi ya miaka kumi, hiki kituko ninachokiona hapa ni cha ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kutoa ushauri wangu kwamba Mheshimiwa Waziri, wenzangu wengi wamelizungumza hili, ninaomba sana iundwe Tume Maalum ambayo itakwenda kila shule kuona vitabu hivi kama vipo sahihi. Pia walimu na Maafisa Elimu wajaribu kuangalia hivi vitabu kabla hawajavinunua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani tulikuwa na utaratibu wale wachapaji na wachapishaji wakiwa wanataka kukuuzia vitabu, lazima wakuletee sample, na wakikuletea sample ni lazima ile sample lazima uipitie kabla hujainunua, jambo la kushangaza ni kwamba hivi vitabu ukiviona hakika ni kituko kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie kuhusu hii Teachers Professional Board, hili jambo limekuwa likizungumzwa kwa muda mrefu sana, ukurasa wa 80 katika hotuba ya Waziri imezungumzia lakini niseme kwa masikitiko makubwa sana hili jambo limeanza kuzungumzwa tangu mwaka 2009 na leo hii tuko 2017. Sasa ndugu zangu kwa kweli hili jambo itabidi kulifanyia haraka kwa sababu nilitegemea kwamba katika Bunge lijalo huu Muswada uwe tabled, lakini inaonyesha kwamba katika huu ukurasa wa 80 kwamba watakamilisha utaratibu wa uwanzishwaji, ina maana kwamba hata taratibu hazijakamilika, hebu naomba niishauri Wizara kuharakisha hii Professional Board ili walau walimu waweze kuona hii Professional Board ili kusudi tuepuke hao walimu ambao wanaingia katika hii fani bila utaratibu maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake pia ukurasa wa 88, kwenye suala la Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo. Niipongeze sana Serikali kwa kuamua kujenga shule ya kisasa kabisa katika Mkoa wa Dodoma, najua kwamba sasa hivi Dodoma ndiyo imekuwa Makao Makuu ya Chama na Serikali, ninapenda tu nimuombe Mheshimiwa Waziri kwamba isiwe shule moja tu, kwa sababu sasa hivi ujio wa watu katika Mkoa wa Dodoma utakuwa ni mkubwa sana. Kwa hiyo, Serikali na Wizara ione isiwe shule moja tu ziwe shule zaidi ili kusudi kuweza ku-accomodate wale watu ambao watakuwa wamefika katika Mkoa wa Dodoma.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo wenzangu wengi wamelizungumzia ni kuhusu elimu ya kujitambua. Niungane na Waheshimiwa Wabunge kwamba suala la mimba za utotoni ni tatizo kubwa sana katika jamii yetu. Sambamba na hilo kila mtu ana mtazamo wake wa kulibeba jambo hili, ila tu ninachoweza kushauri ni kwamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi kuchangia hii hotuba ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote katika kuandaa bajeti hii. Napenda tu nimtaarifu mwanangu Mheshimiwa Halima Mdee kwamba unapokuwa unatoa pongezi ni kwamba unathamini muda na kazi ya mtu ambaye amefanya shughuli hiyo.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tuna kila sababu ya kukupongeza; na kweli katika kuandaa document kama hii siyo kitu cha mchezo. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba kutoa mawazo, kukubali au kukataa kitu, ni haki ya mtu yeyote. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kukusoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna shaka kuwa kilimo ndiyo uti wa mgongo. Waheshimiwa Wabunge wengi wamelichangia hilo. Sambamba na hilo, bila kilimo, viwanda haviwezi kupata malighafi. Hivyo basi, maisha ya Watanzania hayawezi kuwa na tija bila kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirejee, Mkutano wa Maputo ambao ulikutana kuanzia tarehe 10 Julai hadi Disemba, 2003 ambapo viongozi wa Afrika walikutana kwa pamoja na walikubaliana kwamba asilimia 10 za Bajeti za Serikali katika nchi za Afrika ziende katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana, naona kwamba Serikali yetu bado haijafikia lengo hilo na hali kadhalika haijafikia nusu ya lengo hilo; kwamba hadi sasa hivi bajeti yetu ya kilimo ni 4.2% lengo ambalo kwa kweli bado lina hatihati sana. Kwa hiyo, naishauri Serikali yangu sikivu kwamba ione umuhimu wa kuweza kuongeza bajeti ya kilimo kama kweli tunataka kufika katika viwanda vya kati au uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ili wananchi waweze kufaidika kwa kilimo, waweze kujitosheleza kwa chakula na kupata ziada ya kilimo ili wawe na maisha ambayo ni bora, lazima kilimo kitiliwe mkazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa tisa wa hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri, amebainisha kuwa Halmashauri za Wilaya 55 zina upungufu wa chakula kutokana na uhaba wa mvua, lakini hapa hali halisi ni kwamba kwa sababu zinategemea zaidi mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa sana ya wakulima wengi kutegemea mvua kwa ajili ya kilimo ndiyo imesababisha ukosefu wa chakula, mvua ambazo mtawanyiko wake hauridhishi na pengine mvua hizo huzidi na kuleta madhara makubwa ambayo hayana tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wengi wamezungumza na wamebainisha kwamba suluhisho pekee ili tuweze kupata mazao ya kutosha pamoja na usalama wa chakula katika nchi yetu, ni budi tujikite kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kwa hiyo basi, Serikali ina kila sababu ya kuandaa miundombinu rafiki zaidi katika kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia njia mbalimbali zikiwemo kutumia mito ya kudumu, ambayo ninaamini tunayo, mito ya msimu, chemchemi za asili, mabwawa ya kuvuna maji ya mvua na miradi inayotumia visima virefu na vifupi. Naamini kabisa ikiwa Serikali itakuwa na nia ya dhati, tukitumia utaratibu wa umwagiliaji, basi suala la upungufu wa chakula litakuwa ni historia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuongelea ni suala la mbegu na pembejeo. Wenzangu wengi wamelizungumzia, taarifa zilizopo ni kwamba nchi yetu ina uwezo wa kuzalisha mbegu kwa asilimia 35 tu, kiasi ambacho ni kidogo sana. Kwa hiyo, inabidi sasa Serikali ikabuni mkakati mbadala. Hapa nchini tuna vyuo mbalimbali vya MATI, mfano tuna Chuo cha Mlingano - Tanga, tuna Chuo KT - Kilimanjaro, tuna Ukiriguru - Mwanza, Igurusi, Muhongo - Kigoma, MATI - Ifakara na vinginevyo kwa kuvitaja. Hebu Serikali ione jinsi gani itakavyovitumia vyuo hivi kwa kuzalisha mbegu ili mwisho wa siku tatizo la upungufu wa mbegu liweze kupungua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Halmashauri za Wilaya pia zinaweza zikaanda mashamba darasa ya kutosha na hatimaye hili suala la kuagiza mbegu kutoka nje likapungua badala yake mbegu zikawa zinazalishwa humu humu nchini. Wenzetu katika Kamati walishauri kwamba uwepo utaratibu wa kulima kufuata Kanda maalum.

Kwa hiyo, nilikuwa nashauri hata pia katika mbegu, basi ingefanyika utaratibu huo ili kusudi nazo mbegu ziweze kuzalishwa kikanda, nikiamini kabisa na hiyo pia inaweza ikatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Kuzalisha Mbegu, hawa ASA, inabidi nao wajitahidi, waweke malengo makubwa zaidi ili kusudi mbegu ziweze kupatikana kwa wakati na hatimaye suala la kupunguza ukosefu wa mbegu liwe ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu upungufu baadhi ya wataalam, Mabibi na Mabwana Shamba ambao pia imekuwa ni tatizo au kikwazo katika suala zima la kilimo; na hawa wamekuwa na tatizo kubwa sana kwa sababu hawana vitendea kazi vya kutosha. Kukosekana kwa vitendea kazi hivi kunawafanya washindwe kufanya kazi zao kwa ufanisi, hivyo hata kule vijijini ambako wangeweza kwenda kuwasimamia wale wananchi kwa kuwapa utaalamu inakuwa ni tatizo. Kwa hiyo, Serikali ione jinsi gani ya kuwapatia magari, pikipiki, mafuta na vile vifaa ambavyo vinastahiki ili kusudi waweze kufanya kazi zao kwa utaratibu unaotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nililotaka kulizungumzia ni suala la masoko, wenzangu wamelizungumza pia. Pamoja na kwamba baadhi ya wakulima wengi sana wanajitahidi kulima, lakini suala la masoko imekuwa ni tatizo, kwa mfano, katika Mkoa wa Dodoma tunalima sana zabibu, lakini bado soko la zabibu ni dogo. Kwa kweli inabidi tuone Serikali inafanya utaratibu gani kuhakikisha kwamba soko la zabibu tunapata watu wengi zaidi au wawekezaji wengi zaidi ili wawekeze kuweza kusindika mazao ambayo yanatokana na zabibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia, najua muda unanitupa mkono, ni suala la utumiaji wa teknolojia duni. Kwa kweli bado tuna kila sababu ya kuona tunapata wataalam wengi zaidi kwa ajili ya kuwa na teknolojia ambazo ni za kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ukosefu wa zana stadi za kilimo bado wananchi hawajaacha jembe la mkono. Kwa kweli bado jembe la mkono linaturudisha nyuma sana katika kilimo, wananchi wengi hawana uwezo wa kukopa hizi zana za kilimo. Kwa hiyo, bado tuna kila sababu na Serikali ina kila sababu ya kuhakikisha kwamba wananchi wake wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami nichangie mada iliyoko mbele yetu. Kwanza naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuandaa na kuwasilisha Bungeni mapendekezo ya Serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2017/2018. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja moja kwa moja. Katika kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa 47 mpaka 48 Mheshimiwa Waziri amebainisha jinsi Serikali inavyojitahidi kudhibiti mapato kwa kuweka mashine za EFD na pia kuwa na mfumo wa kieletroniki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi zote za Serikali bado kuna baadhi ya wafanya biashara ambao sio waaminifu hawatoi risiti na kuna baadhi ya wananchi wengi bado hawaombi risiti. Hivyo basi, mapato mengi hayaingii katika mfumo ambao tumejiwekea.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana baadhi ya wafanya biashara na wananchi hawafahamu umuhimu wa kodi kwa maendeleo ya Taifa. Nilikuwa napenda kuishauri Serikali yangu sikivu pamoja na Wizara ni budi kwamba hii elimu ya mlipa kodi bado inahitajika sana katika jamii yetu na ikiwezekana iwe ni ajenda ya kuduma na hata ikiwezekana ianzie katika shule za msingi ili wanafunzi wetu waweze kuipata elimu hii ili mwisho wa siku watakapokuwa watu wazima na wao wasiweze kukwepa kodi kwani watafahamu faida ya kodi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa pia ninaomba niongelee kuhusu sekta ya utalii, nidhahiri kwamba sekta ya utalii imekuwa ikiingizia Taifa letu fedha za kigeni na ni sekta ya pili kwa kuingizia Taifa letu fedha za kigeni. Lakini kwa masikitiko makubwa sana katika bajeti hii, katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri halikutiliwa mkazo hili jambo kuhusiana na hii sekta ya utalii. Sambamba na hilo katika hotuba ya Kamati ukurasa wa 40 imebainisha kwamba bado sekta ya utalii inakabiliwa na changamoto za Kisheria pamoja na za kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba utalii ambao uko hapa nchini kwetu ni ule ambao ni high profile tourism ambapo watalii wengi wanaokua hapa nchini wanatumia matumizi yao makubwa zaidi ni pamoja na mahoteli na usafiri. Katika malazi mahoteli mengi sana yanamilikiwa na wageni, hivyo basi pesa nyingi za kigeni haziingii hapa nchini badala yake zinawanufaisha wale wageni katika nchi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa tu naomba niishauri Serikali yangu kwamba hebu ingeweka mkakati wa uhakiki wa kuona ni jinsi gani wazawa wanawezeshwa ili kusudi waweze kumiliki haya mahoteli ili mwisho wa siku, pesa hizi ziweze kubakia hapa hapa nchini na sisi tuweze kufaidika na pesa hizo. Kwa sababu kwa taarifa iliyopo pesa inayobaki kwenye utalii ni pesa kidogo sana ambayo ni hotel levy, pamoja na ile pesa ambayo inatokana na kwenye mishahara ya pay as you earn. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo jambo jingine ambalo katika utalii ni suala zima la usafiri. Usafiri unachukua asilimia 50 ya mapato katika suala zima la utalii, hivyo basi nimpongeze sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuamua kuleta ndege na kulifufua Shirika la Ndege, pamoja na dhamira ya dhati ya kuona kwamba ndege zaidi zinaweza kupatikana, kwa sababu upatikanaji wa ndege hizo utasaidia sana utalii katika nchi hii kwa hiyo kwa vyovyote vile pato la Taifa litaweza kuongezeka kutokana na utalii. Kwa sababu kwa takwimu zilizopo ni kwamba, zaidi ya dola 1.5 bilioni ambazo zimelipa kwenye sekta ya utalii, zimekwenda kwenye usafiri na kwenye usafiri huo waliofaidika zaidi ni mashirika ya ndege ya nje kwa mfano kama Qatar Airways, Emirates na mengine ambayo pia sikuyabainisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba hebu Serikali naendelea kumuombea Mheshimiwa Rais aendelee kufanya kazi kwa bidii sana pamoja na longolongo zote hizi zilizopo, pamoja na maneno ambayo baadhi ya wananchi wanamkatisha tamaa, wenzetu wa upinzani lakini ukweli ni kwamba mwisho wa siku watajua nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais kwa sababu ana nia nzuri sana kwa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba niungane mkono pamoja na wenzangu wote ambao wamenzungumzia kuhusu hii tozo ya shilingi 40 katika mafuta na mimi pia niungane na wenzangu kwamba hebu Serikali ione ni jinsi gani tozo hii sehemu yake ipelekwe katika sekta ya maji ili kusudi tuweze kumtua mwanamke maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la sekta isiyo rasimi napongeza Serikali kwa yote, lakini mimi ushauri wangu ulikuwa ni kwamba ili kusudi tuweze kujua idadi ya watu walioko katika sekta isiyo rasimi, ni vizuri ukafanyika utaratibu wa sensa katika kila Wilaya, katika kila Halmashauri, katika kila Mji au Jiji ili kubaini hao watu wako wangapi, lakini mwisho wa siku ufanyike utaratibu wa watu walioko katika sekta isiyo rasmi waweze kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja na ninashukuru sana kwa kunipa fursa, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote kwa kuandaa hotuba ya Wizara ya makadirio ya Bajeti ya mapato na matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi za Ubalozi zimekuwa na changamoto kubwa ya majengo. Ofisi za Balozi zimepanga ofisi, makazi ya mabalozi na makazi ya maafisa ubalozi. Hakuna eneo, Serikali inamiliki majengo ya balozi zake kwa asilimia mia moja kama tunavyoona baadhi ya nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwezi Serikali inatumia fedha nyingi kulipia kodi. Ikumbukwe kwamba mara nyingi Serikali huchelewesha kupeleka fedha katika Balozi hizi, hivyo kuleta fedheha sana kwa Ofisi za Balozi zilizopo ughaibuni. Nashauri Serikali ikaweke bajeti ili Ofisi zetu za Ubalozi zijenge Ofisi zetu huko nje ya nchi ambako Balozi zetu zinawakilisha. Ni vizuri kodi za pango zikalimbikizwa ili ziweze kujenga majengo badala ya kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Balozi za nchi yetu zilipewa viwanja tangu miaka ya 1980. Nashauri Serikali iweke mkakati wa muda mrefu na mfupi ili kujipanga na kuanza kuendeleza viwanja hivyo. Kama upo uwezekano wa kuviendeleza viwanja hivyo kupitia mikopo ya benki, mortgage finance, higher purchase system na njia nyingine ni budi Serikali ikaona jambo hili na kutekeleza mapema ili majengo hayo yaendelezwe. Tukiacha kuendeleza tunaweza kunyang‘anywa, kwani viwanja vingi vipo katika maeneo maalum (Diplomatic Quarters).

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upungufu wa wafanyakazi nalo ni tatizo kubwa. Ofisi nyingi za Ubalozi zina maafisa wachache sana. Hivi sasa tuna dhana ya diplomasia ya kiuchumi, ni budi Serikali ikaona umuhimu wa kuweka wataalam mbalimbali katika Ofisi za Ubalozi kama wachumi, wanasheria, wenye utaalam wa utalii, Maafisa Uhamiaji ili kuendana na kasi ya diplomasia ya kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wageni wengi wafikao katika shughuli za uwekezaji na shughuli nyingine za kibiashara hukosa taarifa za kutosha kutoka taasisi na Wizara. Nashauri suala la matangazo kwa njia mbalimbali zitumike na hasa njia za mitandao ya kijamii kama facebook, twitter, websites na nyingine nyingi ambao zitaleta tija ili kufanya nchi yetu itambulike zaidi Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kuzipongeza Kamati zote kwa kazi nzuri ya kutoa taarifa ya utekelezaji kuhusu kilimo, mifugo na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kuwa, nchi yetu ilishiriki katika Azimio la Abuja la tarehe 30 Novemba hadi tarehe Disemba Mosi, 2006. Katika Azimio la Abuja kulikuwa na makubaliano kuwa nchi zitenge angalau asilimia 15 ya bajeti za nchi zao katika kilimo. Sisi Tanzania bado tupo chini katika kufikia azimio hilo kuhusu kilimo. Kama ilivyobainisha Taarifa ya Utekelezaji ya Kamati, ukurasa wa sita na saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya nchi za Afrika zikiwemo nchi za Rwanda, Botswana, Nigeria, Malawi, Zambia na Burkina Faso wameweza kutenga bajeti zao za kilimo zaidi ya asilimia 15 ya bajeti zao. Wenzetu Rwanda wameenda mbali zaidi kwa kutenga asilimia 18.8 ya bajeti yake kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaingia katika uchumi wa viwanda na viwanda hivi vinahitaji malighafi itokane na mazao ya kilimo. Je, kwa bajeti ambayo haifiki asilimia 10 tutaweza kufikia huo uchumi wa kati wa viwanda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli napenda kuishawishi Serikali kuona umuhimu wa kuongeza bajeti ili kuleta ufanisi katika kilimo na kuleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kilimo cha umwagiliaji ni miongoni mwa nyenzo muhimu zinazoweza kuleta mapinduzi ya kijani. Suala la utegemezi wa mvua haliwezi kutuvusha kwa jinsi tunavyotaka mapinduzi ya kilimo kwa haraka. Tumeona jinsi mvua zilivyoleta maafa na
mafuriko katika maeneo mbalimbali nchini. Iwapo ungekuwepo utaratibu wa kitaalam wa kuvuna na kuhifadhi maji ya mvua yangeweza kutumika kwa umwagiliaji na hatimaye yangeleta tija. Naishauri Serikali yangu sikivu na Tukufu kuona unafanyika utaratibu wa kuhifadhi maji ya mvua ili yaweze kutumika kipindi cha baadaye na hata ikiwezekana katika kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la utoaji miche ya mikorosho katika Mikoa ya Kanda ya Kati, Dodoma na Singida. Naipongeza Serikali kwa kutoa miche ya korosho. Nashauri ufanyike uhamasishaji wa kutosha kabla ya kipindi cha mvua, ili wananchi waweze kuandaa mashamba ya kupanda miche hiyo. Nashauri miche ya mikorosho itolewe mapema ili wananchi waweze kupata tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami kuchangia katika bajeti hii. Naomba nichukue fursa hii pia kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba nichukue fursa hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii. Naomba nichukue fursa hii pia kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais kwa kutoa kipaumbele kwa afya katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 21 wa hotuba hii Serikali imebainisha ongezeko la maboresho ya vituo vya afya ili kuweza kutoa huduma za dharura. Pia naipongeza sana Serikali Ila napenda kufahamu, pamoja na kutoa huduma za dharura; je, Serikali imejipangaje kwa ajili ya kupata vifaa mbalimbali ikiwemo vifaa vya Ultra Sound, X-Ray sambamba na hilo pamoja na wataalam? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuipongeza Serikali kwa kujitahidi kuongeza uwezo kwa baadhi ya Watendaji wa Idara ya Afya. Naomba niishauri Serikali pia iweke mkakati wa muda mrefu wa kuweza kupata wataalam wa afya zaidi. Kwa sababu wenzangu wengi wamelizungumzia, tuna upungufu mkubwa sana wa wataalam wa afya.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba niishauri Serikali, iandae mkakati wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba wanapatikana watendaji wa afya wengi zaidi kwa kupewa elimu na kutoa kipaumbele ili kusudi waweze kupatikana hawa Watendaji katika Idara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Dodoma, pia na sisi tuna upungufu mkubwa sana wa rasilimali watu na tuna karibu 60%. Kwa hiyo, naomba nitoe shime kwa sababu Mkoa wa Dodoma ni Makao Makuu, hebu Serikali ione iiangalie Mkoa wa Dodoma kwa jicho la kipekee kwa kuwapatia watendaji. Naishukuru tena Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya katika baadhi ya Wilaya za Mkoa wa Dodoma ikiwemo Wilaya ya Chemba, Wilaya ya Chamwino, pamoja na Wilaya ya Bahi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Dodoma imeonekana kwamba kuna ongezeko sasa hivi la maambukizi ya VVU kutoka asilimia 2.9 mwaka 2014/2015 imekwenda kwenye ongezeko la 5% mwaka 2016/2017 wakati kiwango cha Kitaifa kimepungua kutoka asilimia 5.1 kwenda asilimia 4.7. Hii it is alarming kwamba kwa kuwa Dodoma ni Makao Makuu na watu wengi sasa wameanza kuja hapa, hebu Serikali ione umuhimu wa kuwa na mkakati kabambe wa kuhakikisha kwamba maambukizi haya hayaendelei tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda ni mfupi, naomba pia nizungumze kuhusu suala la ukatili ambalo linaendelea kwa kasi sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 97 wa hotuba hii imebainisha kwamba matukio ya ukatili katika mwaka 2016 yalikuwa ni 31,996 wakati mwaka 2017 yamekuwa 41,416. Maana yake ni kwamba matukio ya ukatili yameongezeka kwa matukio 9,420. Hii kwa kweli siyo hali nzuri, ipo sababu sasa jamii pamoja na familia waone jinsi gani ya kulea watoto wetu katika malezi mazuri ili kusudi wasiwe na tabia ya ukatili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nawaomba viongozi wa dini wajaribu kuendelea kuwahubiria wananchi wetu ili kusudi waweze kuwa na mioyo ya uwoga na kumwogopa Mungu ili kusudi kuweza kupunguza huu ukatili. Sambamba na hilo, nilikuwa naomba pia, Serikali ione jinsi gani itafanya kuzuia ukatili badala ya kutoa takwimu nyingi ambazo zinaendelea kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie pia Sera ya Wazee ya mwaka 2003, kwa kweli bado haijatungiwa sheria. Kwa hiyo, nilikuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi nichengie japo kwa dakika tano katika hoja iliyopo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye zao la biashara katika Mkoa wa Dodoma ambalo ni zao la zabibu. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri hakuna katika ukurasa wowote ambako amebainisha kwamba wanatoa kipaumbele gani katika kuendeleza zao la zabibu katika Mkoa wa Dodoma na hii inafahamika kabisa kwamba ni miongoni mwa mazao ambalo linaweza likawakomboa wananchi wa Dodoma katika suala zima la umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha labda anieleze mkakati wa Serikali ni upi wa kuhakikisha kwamba zao hili linaweza likawekewa mkakati maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mbegu za kutosha kwa ajili ya zabibu, lakini sambamba na hilo mbegu za zabibu zinapatikana katika Kituo cha Makutupora. Kituo hiki bado hakina taasisi ya utafiti, kwa hiyo, hata baadhi ya magonjwa ya zabibu hayajulikani. Kwa hiyo, nilikuwa naomba niishauri Serikali yangu tukufu kwamba iione umuhimu wa kuanzisha kituo cha utafiti wa zao la zabibu ili kusudi kuweza kufahamu magonjwa na jinsi gani ya kuweza kupata suluhu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 38 amezungumzia kuhusu Sheria ya Zana za Kilimo. Naomba tu nihamasishe kwamba Serikali imechelewa kuleta sheria hii, hivyo basi hebu ifanye haraka kwani hizi zana za kilimo kwa kweli kuna baadhi ambazo hazikuwa katika ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie pia kuhusu suala zima la alizeti. Mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa mikoa ambayo mvua zake ni chache kwa hiyo mtawanyiko wa mvua ni kidogo. Kwa hiyo, zao la alizeti pia linastahimili katika Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Sambamba na hilo kuna changamoto nyingi, mbegu hazitoshelezi na wakulima wengi wanatumia mbegu ambazo wanakuwa wamezizalisha katika kipindi kilichopita. Kwa hiyo, nilikuwa naomba tu nitoe shime kwa Serikali yangu ione ni jinsi gani itaweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba mbegu za alizeti zinapatikana kwa wakati na zilizo bora ili kusudi tuweze kupata hizo mbegu bora na hatimaye wakulima wetu waweze kupata mazao yenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia hii hoja iliyo mbele yetu ambayo ni hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata fursa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze zaidi kwenye udhibiti wa ubora wa elimu. Nikianzia ukurasa wa 63 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri amebainisha kwamba Wizara imeandaa michoro kwa ajili ya kujenga ofisi 50 za Wadhibiti wa Ubora wa elimu. Naomba tu niishauri Serikali kwamba iharakishe ujenzi wa Ofisi hizi za Wadhibiti Ubora wa Elimu na ikiwezekana basi kwa kuwa Dodoma ni makao makuu na kwenye kitabu chake hiki hakubainisha kwamba ni Wilaya zipi ambazo zitajengewa, basi angetupa kipaumbele sisi Mkoa wa Dodoma kujengewa ofisi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili elimu iwe bora zaidi naamini kabisa masuala ya utendaji wa kazi kwa ajili ya hawa wenzetu wa udhibiti ubora wa elimu yanatakiwa yawe mazuri sana. Katika maeneo mengi ya nchi hii, Wadhibiti wa Ubora wa Elimu hawana kabisa ofisi za kutosha na kama zipo, zipo chache, lakini nyingi ya ofisi hizi ziko katika majengo ambayo ni au yamekodishwa au vipi, kwa hiyo, inawaletea kadhia sana wenzetu hawa. Nikichukulia kwa mfano katika Mkoa wa Dodoma kuna zile Wilaya mpya ambazo zimeanzishwa, katika Wilaya hizi zote hakuna ofisi za Wadhibiti wa Ubora wa Elimu. Kwa hiyo, naomba tu nisisitize juu ya umuhimu wa suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, hawa wenzetu wa Wadhibiti wa Ubora wa Elimu pia nyumba hawana. Sambamba na nyumba lakini pia suala la vitendea kazi, wanahitaji vitendea kazi ili kusudi waweze kutoa taarifa muhimu wanapokuwa wanakwenda kukagua hizi shule. Kwa hiyo, niitie shime Serikali kwamba lazima vitendea kazi vipatikane ili hawa Wadhibiti wa Ubora wa Elimu waweze kuleta mrejesho wanapokuwa wamekwenda kukagua katika hizi shule basi zile shule ambazo zinakaguliwa ziweze kujua wapi zinatakiwa zijirekebishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwenye suala la usafiri katika hizi Ofisi za Udhibiti wa Ubora wa Elimu. Naipongeza Serikali wametoa magari katika baadhi ya hizi Ofisi za Udhibiti wa Ubora wa Elimu lakini tatizo liko kwenye madereva. Bado madereva hawajaajiriwa kwa wingi, utakuta kwamba kuna baadhi ya ofisi inabidi waazime madereva kutoka idara nyingine. Inapotokea kwamba madereva hawa wakaazimwa na yule anajua kabisa kwamba ameazimwa, haoni ni muhimu kuitunza gari ile.

Kwa hiyo, kama imeshindikana basi kuwaajiri hawa madereva, Wizara ione utaratibu itawezaje kufanya itoe kibali maalum ili kusudi kuweza kuwapatia wale Maafisa Udhibiti wa Ubora wa Elimu waweze kuyaendesha wao wenyewe yale magari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie kuhusu suala la OC. OC kwenye Ofisi za Udhibiti wa Ubora wa Elimu kwa kweli imekuwa ni tatizo na hivi ninavyozungumza hata OC ya kuanzia mwezi Januari mpaka hii leo bado hazijapatikana. Tumekuwa tukisema kwamba tunataka elimu iboreshwe, itaboreshwaje ikiwa hawa ndugu zetu ambao wanafanya udhibiti wa ubora wa elimu inakuwa ni mtihani kwao kupata OC? Kwa kweli naomba Wizara ilione hili jambo ili kusudi hawa Wadhibiti wa Elimu waweze kufanya kazi kwa kusimamia suala zima la elimu kwa weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 76 wa hotuba hii imezungumzia kuhusu kuendeleza ujuzi kwa kuboresha vyuo vya ufundi. Naipongeza sana Serikali kwa sababu tutakapopata mafundi mbalimbali kama walivyozungumza wenzangu waliotangulia itasaidia nchi yetu inavyokwenda kwenye uchumi wa viwanda wa kati. Kwa hiyo, suala la ufundi stadi ni la muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe ushauri kwamba katika baadhi ya shule za msingi kuna vituo vya ufundi stadi, hebu Serikali ione jinsi ya kuviboresha vile vituo vya ufundi stadi ambavyo viko katika zile shule za msingi kwa sababu baadhi ya wazazi hawawezi kuwapeleka watoto wao VETA na utakuta vyuo vingi vya VETA viko mijini. Kwa hiyo, Serikali ione itashirikiana vipi na VETA kuweza kuhakikisha kwamba vile vituo ambavyo viko katika shule za msingi vinapatiwa walimu wenye ujuzi pamoja na vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niyapongeze sana taasisi na mashirika mbalimbali ya elimu katika kutekeleza majukumu yake. Niipongeze Serikali kwa kui-task TET iweze kuandaa masuala mbalimbali yanayohusiana na elimu kwa sababu tuliona kabisa kwamba siku za nyuma kumekuwa kukitokea malalamiko kwamba vitabu vya kiada, mihtasari na vinginevyo vimekuwa haviandaliwi kwa maudhui yaliyo sahihi. Kwa hiyo, naomba niipongeze sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi kubwa sana za Serikali katika kuboresha elimu bado tumeona kwamba suala la miundombinu ni changamoto hasa katika shule za Serikali. Mfano, makataba, maabara, vyumba vya madarasa, nyumba za walimu pamoja na samani havitoshelezi. Kwa kuwa Serikali inajitahidi sana kukabiliana na upungufu huu na bado Watanzania wengi wanajitahidi kuzaa kwa kupata watoto wengi, naomba nitoe ushauri kwa Serikali ione umuhimu wa kuhamasisha Halmashauri zote za Miji, Manispaa, Majiji na Wilaya waanzishe mifuko ya kuendeleza elimu katika maeneo yao. Kwa kuanzisha mifuko hii ina maana kwamba itasaidia sasa ku-supplement zile shughuli za Serikali ambazo inawezekana upungufu ni mkubwa ikasaidia kujenga baadhi ya miundombinu na mambo mengine yanayofanana na hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie kuhusu shule binafsi. Wenzangu wengi wamelizungumzia, lakini shule binafsi zinafanya kazi kwa kushirikiana na Serikali siyo competitor, lakini kuna kodi nyingi sana kwa hizi shule za binafsi. Hebu Serikali ione kwamba hawa ni wadau ambao wanakwenda pamoja badala ya kuwawekea hizi kodi nyingi wazipunguze ili kusudi hizi shule za binafsi ziweze kutoa elimu inayotakiwa na tunajua kwamba zinatoa elimu ili wasije wakakwama, wakaona kwamba Serikali inatafuta mbinu ya kuwakwamisha ili wasifikie malengo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie kuhusu wahitimu wa Chuo cha Ukutubi Bagamoyo. Serikali imekuwa ikiingia gharama sana kwa kuwafundisha hawa wakutubi lakini wengi wao hawana kazi na tunasema kwamba vyuo vianzishe maktaba sasa kwa nini hawa wahitimu wasipate fursa hiyo kwa kuajiriwa ili kusudi sasa hizi maktaba ziendeshwe kitaalam? Kwa hiyo, naomba niishauri Serikali ione hilo hitaji kubwa kwamba hawa Wakutubi wanahitajika katika shule ili kusudi waweze kufanya kazi yao kwa jinsi inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba nitoe ushauri kwamba kwenye Ofisi za Udhibiti wa Ubora wa Elimu nako kuwe kuna maktaba maalum na nashauri katika maktaba hizo vitabu vyote vya marejeo, vitabu vya kiada na vitabu vya ziada viwepo ili kusudi viweze kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la vifaa vya kujifunzia na kufundishia bado ni changamoto kwenye mtaala mpya kuanzia darasa la tatu na kuendelea kwa ufundishaji ambao ulikuwa uanze tangu mwaka 2015. Wenzangu wengi wamelizungumzia, lakini kuna baadhi ya walimu wanatumia vitabu vya zamani. Mfano, hisabati darasa la nne havijafika mashuleni na walimu wanatumia vile vitabu vya zamani. Hebu Serikali itafute ufumbuzi wa kuhakikisha kwamba vitabu hivi vya mtaala mpya vinafika shuleni kwa wakati unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, suala la mgawanyo wa fedha bado hauzingatii mahitaji maalum ya shule ambazo zina matokeo mabaya. Tumeona kabisa kwamba kuna baadhi ya shule zina matokeo mabaya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Aidha, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuandaa hotuba hii ya bajeti.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika na wengi tunaifahamu kwamba sekta ya utalii imekuwa ikiingizia pato kubwa sana nchi yetu kwa asilimia 25 pesa ya kigeni. Lakini iwapo sekta hii itafanyiwa marekebisho na ukafanyika usimamizi madhubuti ninaamini kabisa pato hili linaweza likaongezeka zaidi.

Mheshimiwa Spika, wenzangu wamezungumzia kwamba Tanzania ina eneo kubwa sana la fukwe, takribani kilometa 1000 ukianzia Tanga hadi Mtwara. Hata hivyo kwa masikitiko makubwa ni kwamba aina hii ya utalii katika nchi yetu bado haijapewa kipaumbele cha kutosha, kwa hiyo tuna kila sababu ya kutumia tunu hizi.

Nilikuwa naomba niishauri Wizara wafanye utaratibu wa kuwapeleka watalaam wetu katika nchi za Seychelles, Egypt, Tunisia na zile ambazo zimefanikiwa katika utalii huu wa fukwe. Kwa sababu mimi naamini kabisa pia tukiongeza katika utalii wa fukwe pato letu linaweza likaongezeka mara dufu na hivyo sekta hii ikaingiza pesa zaidi.

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa 52 wa hotuba hii umezungumzia pia masuala ya cultural tourism. Napongeza sana juhudi za Serikali kwa kuhamasisha hii cultural tourism. Hata hivyo, pamoja na juhudi hizo bado kuna mambo makubwa sana ya kufanya, kwa sababu mengi sisi nchi yetu haijafanya. Nchi kwa mfano kama Kenya, wenzetu wako hatua kubwa sana, Morocco, Jordan, India pamoja na Uturuki. Katika hili pia nilikuwa natamani niishauri Serikali ifanye utaratibu wa kuona jinsi gani watalaamu wetu wanakwenda kujifunza na kuleta yale mema na sisi tuweze kufanya hii cultural tourism. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia sambamba na hilo na wenzangu baadhi ya wenzangu wamelizungumza, tuna makabila mengi hapa nchini kwetu, nichukulie katika mkoa wa Dodoma. Mkoa wa Dodoma jamii ya Wagogo ni wachezaji wazuri wa ngoma, lakini pia wana utamaduni wao wa kuzungusha shingo ambayo naamini hakuna kabila lingine lolote Tanzania hii wanaoweza kufanya.

Mheshimiwa Spika, sasa kama wakiendelezwa hawa wenyeji wa Mkoa wa Dodoma na wakawa ni kivutio cha utalii mimi naamini kabisa tunaweza tukapata pato kubwa sana. Si wa Dodoma tu, kuna makabila kama Wamakonde wanacheza vizuri sana, Wasukuma, Wanyamwezi, Wangoni, Wafipa, Waha na makabila mengine mengi. Kwa hiyo, iwapo kama utawekwa utaratibu makabila haya yakaonesha mila na desturi zao na tamaduni zao watalii watakuja kwa wingi, mimi naamini kabisa tukikuza jambo hili litatusaidia sana katika hii cultural tourism. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizungumzie kuhusu vyuo vyetu vya utalii, ni vichache sana katika nchi hii. Sambamba na hilo mafunzo ambayo yanatolewa katika vyuo hivi hayaendani na ukuaji wa utalii katika dunia.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba niishauri Serikali kwamba wajaribu kuangalia upya ile mitaala ili kusudi iendane na hali ya sasa hivi. Kwa sababu ukiangalia katika sekta ya utalii Watanzania wengi wanafanya zile kazi za chini, zile kazi ambazo ni za juu hasa katika hoteli za kitalii zinafanywa na wageni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini kabisa tumekuwa na tatizo kubwa sana la ajira, vijana wetu iwapo watapewa mafunzo ya kutosha mimi naamini kabisa hizi nafasi ambazo zinashikwa na wageni badala ya kushikwa na wageni zitachukuliwa na vijana wetu wa Kitanzania. Kwa hiyo, nilikuwa naomba nitoe shime kwa Wizara waone kwamba ili kupata ufumbuzi ni vizuri kurekebisha hili mitaala ili kusudi iendane na mahitaji ya kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa 17 wa hotuba hii Mheshimiwa Waziri amezungumzia kuhusu uwindaji wa kitalii. Ni kweli kabisa kuna baadhi ya vitalu vimetolewa, lakini Serikali imetoa wazo kwamba baada ya shughuli za uwindaji wa kitalii yaani ule msimu ukiisha ufanyike utalii wa picha.

Mheshimiwa Spika, mimi nadhani hili ni wazo zuri sana, lakini pamoja na kuwa wazo zuri hebu sasa Serikali ione jinsi gani itarekebisha miundombinu katika maeneo haya kwa sababu tatizo la miundombinu ni kubwa. Mimi nimekuwa Mkuu wa Wilaya katika eneo la Manyoni na kule kuna Rungwa, Kizigo, Mhesi Game Reserves, lakini miundombinu yake ni mibaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna zile posts ambazo ziko ndani katika haya mapori ya akiba, hebu Serikali ione ni jinsi gani ya kuzirekebisha ziwe katika hali nzuri zaidi ili kusudi wafanyakazi wetu waweze kukaa kule katika yale maeneo ya hizi game reserves. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni jinsi ya kupata taarifa za jinsi watalii wanavyoingia nchini. Mimi nilikuwa napenda kushauri, kwamba ni vizuri kukawa kuna taarifa ambazo zitasaidia ni idadi ya watalii wangapi wameingia nchini, na watalii hawa wametoka katika nchi zipi. Hii itawasaidia baadhi ya wafanyabiashara ambao wanafanyabiashara za utalii wakajua hitaji la soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakitumia social media, tunafahamu kabisa kwamba watu wengi sasa hivi wanatumia social media, kwa hiyo, taarifa hizi zikiwekwa katika social media na watu mbalimbali wakasoma ina maana ya kwamba wale ambao katika nchi zao inaonekana kabisa kwamba utalii upo katika hali ya chini basi hata wafanyabiashara wanaweza wakafanya utaratibu maalumu wa kuona ni jinsi gani wakaweka mkakati kutafuta watalii katika maeneo yale ili sasa kupitia hiyo mitandao ya kijamii tuweze kupata watalii wengi zaidi katika nchi yetu. Sambasamba na hilo tukitumia hivyo inaweza ikatusaidia tukajua kwamba wapi tumejitangaza zaidi na wapi ambapo tunahitaji tujitangaze zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ambalo nilitaka kulizungumzia ni kuhusu professionals katika hizi Balozi zetu nje ya nchi. Nilikuwa napenda niishauri Serikali yangu kwamba kwa kuwa inavyoelekea kwamba utalii ndio unatangazwa lakini haujatangazwa kwa kiwango kile ni vizuri basi kule katika balozi zetu kukawa attached na baadhi ya wataalam ili waweze kusaidia kutangaza utalii. Kwa sababu ukienda maeneo kama Dubai kwa mfano wenzetu wamefanikiwa sana kwenye suala la utalii kwa sababu ya matangazo, wenzangu wengi wamelizungumzia. Kweli matangazo yapo lakini hata hivyo hapa kwetu matangazo hayatoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilikuwa nashauri ikiwezekana Serikali iweke utaratibu wa kupeleka professionals katika balozi zetu mbalimbali ili waweze kusaidia kutangaza utalii wa nchi yetu na hatimaye tuweze kupata…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata fursa ya kuchangia kwa maandishi. Aidha, nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote walioandaa hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kuwa ofisi za Ubalozi zimepewa jukumu la kutoa Visa kwa wageni mbalimbali wanaotaka kufika nchini kwa shughuli mbalimbali, suala la Visa rejea. Katika utoaji wa Visa rejea kumekuwa na ucheleweshaji sana kuwapata waombaji wanaotoka katika zile nchi ambazo nchi yetu inawapatia Visa hizo. Kuna nyakati Visa rejea hutolewa baada ya miezi mitatu na wakati mwingine waombaji hawapati majibu kabisa. Hii inaleta adha kwa wale wageni wanaotaka kuja pamoja na Maafisa Balozi. Hali ya kuchelewa au kutopata Visa rejea, husababisha Serikali kukosa mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kulipitia upya sharti la Visa rejea ili kwenda na wakati kwa kufungua milango ili wageni waweze kuingia. Mfano watalii, wawekezaji, wafanyabiashara na wageni wengine ambao huja kwa shughuli za mikutano na ziara za utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, malipo ya ada ya Visa kuwa juu na kwa dola. Kuna baadhi ya mawakala wamekuwa wakitoa pesa juu sana kwa ajili ya Visa mfano baadhi ya mawakala wa Saudi Arabia wamekuwa wakitoza ada si chini ya dola 600, sambamba na hilo kuna baadhi ya mawakala hawana ofisi maalum, ni budi Wizara kufanya uhakiki wa mawakala wote ili kuwaondolea adha Watanzania kulanguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 66 ajira mpya, pamoja na kupata kibali cha kuajiri watumishi 10 bado ofisi nyingi za Ubalozi zina upungufu wa wafanyakazi wanadiplomasia. Hebu Serikali ifanyie kazi ili wapatikane na kutosheleza ili kuleta ufanisi katika utendaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafasi za kazi nje ya nchi. Tanzania imekuwa ikisisitiza umuhimu wa Watanzania wana diaspora waishio nje kuchangia uchumi wa Taifa letu kwa kuleta mapato wapatayo huko ughaibuni. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha jambo hili linaenda sawa na kuleta tija kwa nchi? Mkakati upoje ili Watanzania wote waishio ughaibuni wafahamike wapo nchi zipi na wanafanya kazi au shughuli zipi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia kwa maandishi na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa. Waziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba iliyosheheni taarifa muhimu za utekelezaji kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi na pia kuandaa bajeti yenye dhamira ya dhati ya kuleta maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Mawaziri wote, Naibu Mawaziri pamoja na watendaji wote walioshiriki kuandaa taarifa ya bajeti hii. Wananchi wamejenga maboma mengi ya zahanati na wamefikia hatua mbalimbali na wamekuwa wakihitaji msaada kutoka Serikalini ili kukamilisha maboma hayo kwa ajili ya kupunguza mwendo kwenda kupata huduma za afya. Natoa rai katika bajeti hii Serikali iweke fedha kwa ajili ya kukamilisha baadhi ya zahanati. Aidha, nashauri uwepo mpango maalum wa Serikali na kujiwekea ratiba maalum ili kukamilisha maboma haya ya wananchi hatua kwa hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi ya visima vya maji imekwama kutokana na miundombinu. Visima vimechimbwa lakini baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Dodoma pump na mitambo hakuna. Ni budi Serikali ikayabaini maeneo yote nchini yenye kadhia hii na kuona jinsi ya kurekebisha ili wananchi waweze kufaidika na upatikanaji maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tumepitisha sheria inayoitaka kila Halmashauri itoe asilimia 10 ya mapato kwa makundi ya wanawake, vijana na walemavu. Nashauri Serikali ifanye ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha kila Halmashauri inatekeleza pia urejeshwaji wa pesa hizo. Aidha, ifanyike tathmini mwishoni mwa mwaka wa fedha kuona wananchi waliofaidika wamebadilika vipi kupambana na umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni budi uwekwe utaratibu wa utoaji taarifa kuhusiana na asilimia 10, ikiwezekana kila Halmashauri iwe inatoa taarifa ya maendeleo ya utoaji na urejeshaji fedha kila baada ya miezi sita au jinsi Serikali itakavyoona inafaa. Hali kadhalika Maendeleo ya Jamii wapitie Halmashauri zote zisizofanya vizuri ili zichukuliwe hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika michezo kuanzia ukurasa wa 71-73 imezungumzia soka, je, timu za soka la wanawake hawakushiriki katika michezo? Michezo ya mpira wa pete na mingine inayochezwa na wanawake nayo ipewe kipaumbele ili kuonyesha pia wanawake wanashiriki soka na michezo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza uwepo wa ziada ya chakula ya tani milioni 3.32 za mazao yetu. Aidha, kipindi hiki mvua si nzuri na ukame umeathiri maeneo mengi, hivyo suala kilimo cha umwagiliaji bado inabidi Serikali ilisisitize kwani kutegemea mvua bado si salama kwa usalama wa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hii hoja iliyopo mbele yetu. Pia naomba nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa Mambo Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Kangi Lugola pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa hotuba hii ambayo wameiandaa.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, naomba niwapongeze Askari Polisi wote kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kuitetea na kuilinda nchi yetu. Hali kadhalika nawapongeza Majeshi ya Magereza, Idara ya Uhamiaji, NIDA na Jeshi la Zimamoto tunaelewa wanafanya kazi yao nzuri pamoja na ufinyu wa bajeti iliyopo, pongezi zao sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kujitahidi kuboresha ustawi wa Jeshi la Polisi kwa kuona umuhimu kwanza wa kuboresha ukarabati wa Chuo cha Taaluma cha Polisi, Dar es Saalam, lakini pia na ujenzi wa nyumba za Jeshi la Polisi pamoja na Askari Magereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze kuhusu suala la usalama barabarani nikirejea ukurasa wa tisa hadi wa 10 katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Imebainisha kwamba sasa hivi ajali zimepungua kwa asilimia 38, napongeza hatua hiyo. Sambamba na hilo, naomba nichukue fursa hii kuiomba Serikali yangu Tukufu kuona umuhimu sasa wa kuipitia Sheria ya Usalama Barabarani kwani bado ina upungufu mwingi na upungufu huu iwapo kama utaondolewa ina maana kwamba tutawalinda wananchi wetu waweze kuepukana na vifo pamoja na ulemavu wa kudumu.

Mheshimiwa Spika, naungana na maoni ya Kamati yangu, na-declare interest mimi ni mjumbe wa Kamati hii, kwamba kuiomba Serikali iharakishe marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani, Sura 168 kwani hatuoni sababu kwa nini inachelewa. Kwa sababu tukirekebisha sheria hii kuna baadhi ya mambo ambayo yanaweza yakaleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nataka kujua, kwa nini Serikali imechelewesha kuleta marekebisho ya sheria hii, kwa sababu sasa hivi kumekuwa kuna matumizi ya teknolojia na baadhi ya madereva wetu wamekuwa hawafuati Sheria za Usalama Barabarani kwa sababu wanaendesha vile vyombo vya moto huku wakitumia simu. Kwa hiyo wanapokuwa wakitumia simu hizi ina maana kwamba umakini wao katika kuendesha vyombo hivi unakuwa ni mdogo sana. Kwa hiyo kama ikipatikana Sheria ina maana kwamba itawabana hawa madereva ambao ni wazembe na itasaidi kupunguza ajali.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo katika kurekebisha sheria hii, naamini kabisa hili suala la kiwango cha kilevi ambalo liko katika sSheria ya nchi yetu kwamba madereva wanaruhusiwa kuwa na asilimia 0.08 ya kiwango cha kilevi. Je, kwa nini Serikali isione umuhimu sasa wa kubadilisha kiwango hiki ili kiwe asilimia 0.05 ambacho kinaendana na kiwango cha kimataifa chini ya World Health Organization. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa 17 wa hotuba hii, Waziri amezungumzia kuhusu kuongeza rasilimali watu na fedha na kubainisha kwamba, kuna baadhi ya maaskari wamehitimu mafunzo. Ningependa kujua, Je, katika mafunzo haya kuna jicho la kijinsia? Ni wanawake wangapi ambao wamepata fursa ya kwenda katika mafunzo haya na kupandishwa vyeo katika maeneo mbalimbali. Kwa sababu naamini kabisa sote tunafahamu kwamba nchi yetu imeridhia matamko mbalimbali ya kuhakikisha kwamba usawa wa kijinsia unakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna malalamiko ya baadhi ya Maafisa au Polisi (askari) wa kike ambapo wakipangiwa mafunzo na ikitokea bahati nzuri wakawa wajawazito…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Muda hauko upande wako Mheshimiwa Toufiq.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshmiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata muda wa kuchangia kwa maandishi. Kumekuwa na mamalamiko kutoka kwa baadhi ya maaskari wa kike kutopangwa mafunzo ikitokea bahati nzuri askari huyo ni mjamzito. Aidha, nafasi ya vyeo kwa wanawake inaonyesha bado ni finyu. Je, Jeshi la Polisi linawapa fursa gani maaskari polisi wanawake wanaoahirisha mafunzo kutokana ujauzito na fursa zipi za mafunzo hupata maaskari hasa baada ya kujifungua?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono maoni ya Kamati kuendelea kutoa msisitizo kwa Serikali kutoa fedha kwa wakati ili kuimarisha utendaji kazi na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa mafunzo 14,28,51 na 93.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa mchango wa maandishi kuhusu tohara ya kitabibu na natambua juhudi za Serikali katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na wanaume wengi kujitokeza kufanya tohara lakini bado baadhi wanaona aibu, nashauri campaign iendelee pia kwa kuwashirikisha wale wanaume waliofanyiwa tohara wakiwa na umri mkubwa na pia Wabunge na viongozi wanaotoka maeneo yasiyofanya tohara kwa wanaume wafanye campaign hiyo ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU. Hali kadhalika ushauri utolewe kuwa watoto wa kiume watahiriwe wakiwa wadogo ili kuwaondolea kadhia ya kutahiriwa katika umri mkubwa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami kuchangia hii hoja iliyopo mbele yetu. Naomba nichukue fursa hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2019/2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii pia kuungana mkono na Wabunge wote wa chama tawala na watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi hii kwa kumpongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa elimu bure ambayo pia ni lengo namba nne la maendeleo endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilichangia bajeti ya elimu, naomba nichukue fursa hii kuishukuru sana Serikali yangu kwa kutekeleza baadhi ya maombi ambayo sisi kama Wabunge tuliomba Serikali hii iyafanye. Nikichukulia mfano katika Mkoa wa Dodoma, mazingira ya utendaji kazi katika udhibiti wa elimu kwamba Wizara imetoa kiasi cha milioni 152 kwa ajili ya Wilaya za Chemba, Bahi, Chamwino na Jiji kwa ajili ya kujenga Ofisi za Wadhibiti Ubora wa Elimu, pongezi sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, pia zimetolewa fedha kwa ajili ya ukarabati wa Ofisi za Udhibiti Ubora wa Elimu katika Wilaya za Kongwa na Mpwapwa. Naomba niwatie shime, niwatie shime watendaji wa Wizara chini ya uongozi wa Waziri, pamoja na kelele zote ambazo mnaambiwa kwamba Serikali haijafanya kitu kwenye suala la elimu naomba mtembee kifua mbele watanzania tuko pamoja na ninyi, mnafanya kazi nzuri sana pamoja na ufinyu wa bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ambayo nilikuwa naomba niishauri Wizara ijaribu kuona inaifanyia kazi, hasa kwa suala la watumishi wa walimu waliopo Wizara ya Elimu, wengi wamekuwa wakicheleweshewa kupandishiwa madaraja kwa muda mrefu. Nikichukulia kwa mfano, mwalimu aliyeanza kazi TAMISEMI mwaka mmoja pamoja na mwalimu aliyeanza kazi Wizara ya Elimu ngazi zao za mishahara zinatofautiana. Kwamba huyu wa TAMISEMI yuko TGTS I, wakati wa Wizara ya Elimu TGTS G, hii inapunguza sana ari ya utendaji wa kazi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri hili mlione ili kusudi sasa muweze kuwapandisha waalimu hawa madaraja kwa muda ambao unaotakiwa. Kwa sababu imetokea pia kuna baadhi hata wakati wa kustaafu wamekuwa wakitofautiana kupata yale mafao kwa hiyo hii inakuwa inawakatisha sana tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nilipenda kufahamu kwanini Wadhibiti Ubora wa Elimu hawapati posho ya madaraka? Kwa sababu wao ndiyo wanaokuwa wakiwakagua hawa waalimu katika shule lakini cha kushangaza ni Waalimu Wakuu, Waratibu Elimu Kata ndiyo wanaopata posho. Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake, nilikuwa naomba ajaribu kunieleza, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba Wadhibiti Ubora katika ngazi ya wilaya na ngazi ya kanda nao wanaweza kupata fursa ya kuweza kupata posho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 129 hadi 130 ya hotuba hii amezungumzia kuhusiana na suala la elimu ya ufundi, kwamba Wizara ina mpango wa uendelezaji wa elimu ya fundi study kwa muda mrefu ambao watatoa washiriki 10000 lakini kwa muda mfupi watakuwepo washiriki 24000. Ushauri wangu kwa Wizara, kwa kuwa kuna baadhi ya shule za msingi zina vituo vya ufundi study, hebu Wizara ione kwamba vituo hivi vifufuliwe wapewe walimu wawepo, vifaa viwepo pamoja na bajeti iandaliwe ili kusudi vituo hivi viweze kufanya kazi kwani vina msaada mkubwa sana katika maeneo ya vijijini. Kutokana na vituo hivi tunaweza tukapata mafundi mbalimbali kutoka hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 25 wa hotuba hii pia Waziri amezungumzia kuhusu suala la kuimarisha study za utoaji ushauri na unasihi kwamba kuna waalimu 300 watapewa mafunzo hayo. Nilikuwa naomba niishauri Serikali kwamba hawa walimu wawe wengi zaidi kwa sababu suala la ushauri na unasihi linahitajika sana kuanzia shule za msingi hadi shule za sekondari na hadi vyuo. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali iangalie kwa upya zaidi na kuongeza bajeti katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nilikuwa naomba nizungumzie kuhusu elimu maalum. Sisi katika Mkoa wa Dodoma tuna Shule ya Buigiri, wasiiona. Nilikuwa niiombe Wizara waone sasa umuhimu wa kuweza kutupatia vitabu vya kutosha hasa vile vya nukta nundu kwa sababu bado kuna upungufu wa vitabu hivi ili watoto wetu waweze kupata elimu iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upungufu wa waalimu wengi wamelizungumzia, na mimi naomba nilizungumzie…

MWENYEKITI: Kengele ya pili tayari, malizia.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Hili ni tatizo la kitaifa, lakini pia upatikanaji wa fedha za kutosheleza. Baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa na mimi fursa ili niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nami niungane na wenzangu wote kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wetu Bi. Ummy Mwalimu, lakini pia nimpongeze Naibu Waziri, Dkt. Faustine Ndugulile. Watendaji wote, Katibu Mkuu wa Afya, mdogo wangu Dkt. Zainabu Chaula, pongezi sana pamoja na Katibu Mkuu wa Maendeleo ya Jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niungane na maoni ya Kamati kwamba fedha zote ambazo hazijakamilishwa kutolewa katika Wizara hii zitolewe kwa wakati ili kusudi waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 121 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia kuhusu mpango mkakati wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto 2017/2018 hadi 2021/2022. Naipongeza sana Serikali kwa kuratibu na kuanzisha hizi Kamati za Ulinzi wa Watoto na Wanawake na inasemekana mpaka sasa hivi Kamati hizi zimefikia 7,383. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, napenda tu kufahamu kwamba Wizara imejiandaaje katika kuhakikisha kwamba mpango huu unafahamika zaidi katika jamii yetu hasa kule pembezoni. Kwa sababu mpango huu dhima yake najua ni nzuri sana kuhakikisha kwamba wanawake na watoto wanakuwa hawafanyiwi ukatili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kufahamu Serikali ina mkakati gani wa kutunga sheria ya jinsia ili kusudi sasa iweze kuangalia masuala yote kwa jicho la kijinsia. Kama tukiwa na sheria hii naamini kabisa masuala mengi ya kijinsia yanaweza yakafanyiwa utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tafiti zimebainisha kwamba ukatili unaanzia majumbani na wengi wanaofanyia watu ukatili ni ndugu wa karibu. Wizara imejipangaje kuelimisha jamii kuhusiana na suala hili ili kusudi watu wasione tabu kulizungumzia na hatimaye wahusika wanaofanya ukatili waweze kuchukuliwa hatua zinazostahiki? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie kuhusu ustawi wa wazee, wenzangu wengi wamezungumzia. Suala la ile sheria na mimi pia naomba nisisitize kwamba sheria inabidi itungwe kwa sababu nchi yetu imeridhia matamko mbalimbali lakini pia mwaka 2016 Umoja wa Afrika ulikuwa umekubaliana kupitisha mwongozo kuhusu haki za wazee lakini inaelekea kwamba nchi yetu bado haijaridhia makubaliano hayo. Naomba basi ifanyike ili kusudi wazee wetu waweze kupata tija, kwa kweli wazee nao wanahitaji fursa nyingi na mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie kuhusu makao ya wazee. Kwa kweli kuna changamoto kubwa sana, haya makao ya wazee 17 ambayo ni ya Serikali bado yako katika hali mbaya sana. Naomba Serikali ifanye matengenezo yanayohitajika ili kusudi hadhi ya wazee iweze kupatikana kwa sababu inaonekana kwamba wazee wameachwa nyuma sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu masuala ya makuzi ya watoto, hii imezungumziwa katika ukurasa wa 123 hadi 132 katika hotuba hii. Sasa hivi watoto wengi sana ambao tulikuwa tukiwategemea wawe mayaya au walezi wanakwenda kusoma shule. Kwa sababu ya elimu bure watoto wengi wa kike siku hizi tena hawaendi kufanya kazi za majumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilichokuwa naomba nishauri ni kwamba Serikali ione utaratibu wa kufanya ili kusudi viwepo vituo vingi vya malezi ya watoto wakati wa mchana ili kusudi sasa wazazi na walezi waweze kuwapeleka watoto wao katika vituo hivi. Watoto kwa kukaa katika vituo hivi ni ili ustawi wa wale wao uwepo lakini pia waweze kuwa katika mazingira salama. Vituo hivi vitumike kama sehemu bora ya ulinzi na usalama wa watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nizungumzie kuhusu suala la afya ya kinywa na meno. Tatizo ni kwamba sasa hivi watu wengi sana wamekuwa na tatizo hili la afya ya kinywa na meno Serikali ituambie ina mkakati gani wa kwanza kuzuia ili kusudi watu wengi wasipate madhara na pia wataalam wengi wa masuala ya kinywa nao pia wapatikane. Kwa sababu inaonekana kwamba maeneo mengi wataalam hao hawapo, kwa hiyo, wananchi wanapata shida sana kwa ajili ya afya ya kinywa na meno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa fursa ya kuchangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, ushauri kuhusu uanzishaji wa Madawati ya Jinsia katika Taasisi za Vyuo Vikuu na Vyuo vya Kati, niipongeza Serikali kwa kuanzisha madawati haya. Mwongozo huu utasaidia wanafunzi kupata ushauri na pia inaweza ikawanusuru changamoto za msongo wa mawazo, kuua na kujiua, rushwa ya ngono na masuala mengine ya ukatili. Ushauri wangu mwongozo huu uwe popularized katika vyuo vyote. Pia wanavyuo wote wafahamishwe kuhusu mwongozo huu. Pia Serikali iongeze bajeti ya maendeleo Fungu 53 katika pesa ya maendeleo ili kuleta ufanisi.

Mheshimiwa Spika, ushauri kuhusu ukatili kwa watoto; watoto wafundishwe kutoa taarifa na wasiogope vitisho wanapofanyiwa ukatili watoe taarifa, pia wazazi/walezi wawe wanakagua watoto wao kuona kama wamefanyiwa ukatili na kuchukua hatua za mapema.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa fursa ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ambayo ni Hotuba ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Kigwangalla, Naibu Waziri, Mheshimiwa Kanyasu Constantine na Watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii tunayoijadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza mafanikio ya Wizara kama ilivyobainishwa katika ukurasa namba 10 hadi 18 wa hotuba, ikiwemo kupungua kwa ujangili, uanzishwaji Jeshi Usu, kubadilisha hadhi baadhi ya maeneo ya hifadhi, ongezeko la watalii, mapato na kadhalika. Pamoja na mafanikio yaliyopo bado kuna changamoto ambazo zikipatiwa ufumbuzi zitaleta tija na ufanisi katika utendaji wa Sekta ya Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, iwapo Serikali itatoa fedha iliyoidhinishwa yote na kwa wakati ni dhahiri miradi iliyokusudiwa itatekelezwa, kuna wakati na kuiletea pato kubwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Suala la Biashara ya uwindaji wa Kitalii ni tofauti na biashara nyingine, ni ukweli usiopingika uwindaji wa kitalii unahitaji amani, uwepo wa vivutio vyenye sifa ili wawindaji wa kitalii waendelee kuja na kuliongezea Taifa kipato, Wizara iwe na mikakati endelevu ya kuwezesha biashara ya uwindaji wa kitalii ishamiri, pia mazingira ya wanyama stahiki yalindwe vema, kwani kuna baadhi ya wananchi wanavamia maeneo ya mapitio ya wanyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Idara ya Misitu na Nyuki, Wakala wa Misitu (TFS) nina ushauri ufuatao: Uwepo uhifadhi wa misitu wenye tija, kwani uhifadhi misitu, si utaalam tu bali ni pamoja na matumizi endelevu ya misitu, bila kupoteza sehemu yoyote ya malighafi hususan na kuzingatia utaalam wa teknolojia ya kisasa katika uhifadhi misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado usimamizi wa Misitu haukidhi viwango na misingi inayolenga kuendeleza uchumi wa nchi na uboreshaji mazingira, mfano mashamba ya miti, Tanzania ina maeneo makubwa lakini kasi ya upandaji miti si wa kasi sana. Kasi ya upandaji miti na uvunaji haziwiani hivyo kutishia uvunaji endelevu, hasa miti ya asili. Miti ya asili inazidi kupotea, ni budi Serikali kupitia Wizara ikawe na utaratibu wa kuelimisha watoto, vijana na jamii kwa kuwapa elimu kuhusu umuhimu wa misitu katika maendeleo ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Misitu katika mabonde na mito nayo wananchi waelimishwe umuhimu wake. Katika mazao ya Nyuki, nampongeza Mheshimiwa Mizengo Pinda, Waziri Mkuu Mstaafu na wadau wengine wote wanaoendeleza zao la nyuki, ni zao ambalo linaweza kuleta mapinduzi makubwa kiuchumi, hivyo wananchi wengi wahamasishwe ili wajiingize katika biashara ya mazao ya nyuki pamoja na uhifadhi wa mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iendelee kuwaelimisha hasa wananchi wa pembezoni na vijijini faida ya mazao ya nyuki badala ya kuharibu mazingira kwa kuchoma mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kusisitiza Wizara ijikite kwa undani katika masuala ya utalii na fukwe, mapango, mila na desturi za makabila, historia ya Viongozi wa kimila na makabila mbalimbali Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami kuchangia hoja iliyo mbele yetu katika hili Bunge lako Tukufu. Kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, mwingi wa ukarimu kwa kunipa uhai wa kuweza kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Spika, naomba niungane na Wabunge wenzangu wote kwa ajili ya kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri wote pamoja na watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii. Kazi ambayo imefanywa na uongozi chini ya uongozi wa Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli inaonekana. Tunachotakiwa sisi ni kuendelea kumtia moyo, kumpongeza, pamoja na wale wote ambao wameunda timu kuhakikisha kwamba, Tanzania yetu inafikia ile azma ambayo wamejiwekea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nizungumzie kuhusiana na suala kwanza la ugonjwa huu wa corona. Wenzangu wengi wamelizungumzia, niungane na wenzangu kutoa pole kwa Watanzania wenzangu ambao Ndugu zao wamepatwa na ugonjwa huu, lakini pia ambao wameondokewa. Niipongeze sana Serikali kwa juhudi kubwa sana ambayo inaifanya kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, wananchi wanapata elimu ya kutosha kuhusiana na ugonjwa huu.

Mheshimiwa Spika, lakini bado suala la misongamano lipo na hii inaweza ikaleta athari kwa baadhi ya maeneo. Sambamba na hilo elimu katika maeneo ya pembezoni inahitajika sana, Ndugu zetu wa vijijini bado hawana elimu ya kutosha kwa hiyo, nilikuwa naomba nitoe rai kwa Serikali pamoja na Wizara tuone ni jinsi gani elimu katika maeneo ya pembezoni inafika, ili kusudi Wananchi hawa waweze kujikinga na huu ugonjwa hatari ambao umeleta maafa makubwa sana katika dunia yetu.

Mheshimiwa Spika, ugonjwa huu wa corona umesababisha baadhi ya wafanyabiashara hali ya biashara zao kudorora. Nichukulie kwa mfano, najua kwamba nia nzuri sana ya Serikali kufunga vyuo, kufunga shule, hii ilikuwa ni katika kuhakikisha kwamba, huu ugonjwa hauenei, lakini sambamba na hilo sasa kuna baadhi ya wafanyabiashara ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa kuzihudumia taasisi hizi. Wafanyabiashara hawa sasa biashara zao kwa kweli, zimedorora na kuna baadhi yao wamechukua mikopo. Je, Serikali inaona hawa watu itawasadia kiasi gani kwa sababu, katika kipindi hiki cha mpito ambacho sasa hili janga linaendelea kuwepo na hawa baadhi ya wafanyabiashara wengine waliochukua mikopo benki. Sasa nilikuwa naiomba Serikali ijaribu kuona itawasaidiaje hawa watu, ili kusudi sasa baada ya hiki kipindi cha mpito waweze kuendelea na shughuli zao.

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa 26 wa hotuba hii umezungumzia kuhusu shughuli zilizochangia ukuaji wa pato la Taifa ambao umefikia 6.9%. Niipongeze sana Serikali yangu kwa jinsi inavyofanya kazi nzuri ya ukusanyaji wa mapato, lakini sambamba na hilo kuna kundi ambalo natamani kundi hili kwa mfano Serikali imekuwa ikitoa mikopo kwa makundi ya vijana, makundi ya wanawake, watu wenye ulemavu, lakini pia na wajasiriamali mbalimbali. Nilitamni nione kwamba, hawa nao tunaona wanachangiaje katika pato letu la Taifa, ili mwisho wa siku na wenyewe nao ufanyike utaratibu, kama ni tathmini, au utafiti waweze kuweza kuchangia katika hili pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizungumzie kwenye issue ya utalii. Naipongeza sana Serikali kwamba, katika hotuba hii kumekuwa na matangazo mengi sana ya vivutio vya utalii katika maeneo mbalimbali, lakini Serikali imebainisha kuwa kuna mkakati wa kuwekeza zaidi katika utalii na hasa katika utalii wa fukwe, utalii wa meli, utalii wa mkutano, utamaduni, mali kale, ikolojia na jiolojia. Nilikuwa naomba niishauri Serikali kwamba, mkakati huu uendane pia na kupatikana na wataalam ambao wataweza kusimamia aina hii ya utalii. Ninaamini kabisa kama tukiwa tuna wataalam wa kutosha basi utalii huu utaleta tija kubwa sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie pia suala la UKIMWI. Nimesikia wenzangu wengi wamelizungumza na tunafahamu kwamba Serikali imejitahidi sana naipongeza sana kwa kufanya kampeni kubwa sana. Zimefanyika kampeni kubwa sana katika kuhakikisha kwamba UKIMWI unapungua au unakwisha kabisa. Hata hivyo, kuna hii AIDS Trust Fund, nashauri Mfuko huu tuone tunafanya utaratibu gani wa kuweza kupata rasilimali za kutosha. Kutokana na taarifa zilizopo ni kwamba hawa wafadhili ambao wamekuwa wakitoa ufadhili kwa ajili ya dawa na kadhalika wameanza kupungua.

Mheshimiwa Spika, naona kama litapatikana tozo la kuweza kusaidia Mfuko huu ukatunishwa, ina maana kwamba sisi wenyewe kama nchi tutaweza kujitegemea na hivyo suala zima la prevention na mambo mengine ambayo yanahusiana na hayo Mfuko huu utaweza kusaidia. Hivyo, kupitia makampuni mbalimbali kama ya simu au pengine taasisi mbalimbali ambazo zimekuwa zikifanya miradi mbalimbali tunaweza tukawawekewa utaratibu maalum wa kuwa na tozo maalum kwa ajili ya Mfuko huu, naamini kabisa nayo hiyo inaweza ikasaidia.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kushauri ni kuhusiana na suala zima la mkakati wa behavioral change kwa ajili ya vijana wetu kuanzia miaka 15 – 24 kwa sababu inaonekana kwamba hili ni kundi kubwa ambalo limekuwa likiathirika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ni kuhusiana na ukuzaji wa lugha ya Kiswahili. Kwanza nipongeze sana Mkutano wa Wakuu wa nchi wa SADC kwa kuamua kwamba Kiswahili kiwe ni mojawapo ya lugha rasmi katika mikutano hiyo. Sambamba na hilo, imeonesha kwamba bado wataalam wa Kiswahili tunao wachache sana. Kutokana na taarifa iliyopo katika ukurasa 104 wa hotuba hii, imebainika kwamba wataalam waliopo wa Kiswahili ambao wamesajiliwa ni 1,159. Hii ni idadi ndogo sana, kwa hiyo naiomba Serikali basi vijana wengi zaidi wahamasishwe ili kusudi wawe wataalam wa Kiswahili na hatimaye waweze kutangaza Kiswahili chetu katika nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, najua muda sio rafiki sana naomba nizungumzie kuhusiana na suala la mikopo kwa elimu ya juu. Ukurasa wa 66 unazungumzia kuhusu mikopo, niipongeze Serikali kwa ule wigo kuwa mkubwa wa upatikanaji wa mikopo. Kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya hawa wanufaika wa mikopo kwamba hii mikopo wakati wa urejeshaji kumekuwa na sintofahamu. Kwa mfano utakuta kwamba pengine mtumishi au kijana katika salary slip yake inaonesha kwamba ile outstanding loan ni milioni 20 lakini akienda kule Bodi ya Mikopo anakuta outstanding loan ni milioni 24. Kwa hiyo natamani labda ungefanyika utaratibu wa kuhakikisha haya madeni ili kusudi hawa vijana wetu wasije wakaona kwamba kuchukua mkopo imekuwa ni burden kubwa sana kwao. Kwa hiyo akianza kufanya kazi ile pesa nyingi inachukuliwa, kwa hiyo naomba Serikali ijaribu kuona jinsi gani itaweza kuangalia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai wa kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Sambamba na hilo, naomba nikushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 hadi 2025/ 2026.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Wizara husika, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote kwa kuandaa Mpango huu. Niwapongeze pia ndugu zetu wa Kamati ya Bajeti kwa kuandaa taarifa yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze moja kwa moja kwenye hoja ambayo ningependa kuizungumzia leo, miongoni mwa hoja hiyo ni pamoja na kilimo cha umwagiliaji. Waheshimiwa Wabunge wengi wamelizungumzia hili suala la kilimo cha umwagiliaji nami pia naomba nichangie kwenye suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kujengwa na kuboreshwa kwa miundombinu ya umwagiliaji kulingana na Taarifa ya Mpango kwamba kutoka hekta 461,372 mwaka 2015 hadi kufikia hekta 694,715 mwaka 2020 bado kilimo cha umwagiliaji kinahitaji kufanyiwa kazi ya ziada. Nilitamani tungepata maelezo kwamba hizi hekta 694,713 zilifikiwa kwa lengo lipi, kwamba je, Serikali ilikuwa imepanga kufikia lengo kiasi gani katika suala zima la kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu ambazo nimezifuatilia inabainisha kwamba tuna zaidi ya hekari milioni 29 ambazo zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Hata hivyo, hadi sasa ambazo zimeweza kufanyiwa kazi yaani katika kilimo cha umwagiliaji ni hizi hekta 694,715. Leo ni miaka 50 na zaidi ya uhuru, kwa kweli kiwango hiki cha hekta hizi bado tuna safari ndefu sana kama tunahitaji mapinduzi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomb nitoe rai kwamba tuone jinsi gani Serikali inajipanga vizuri kuhakikisha kwamba kilimo cha umwagiliaji kinawekewa uwekezaji mkubwa ili kusudi tuweze kupata chakula cha ndani ziada, mazao ya biashara na ili kusudi tuweze kuuza katika masoko ya nje. Leo nakumbuka asubuhi wakati Mheshimiwa Bashe akijibu swali la Mheshimiwa Timotheo Mnzava alizungumzia kwamba katika Mpango huu wana-plan kufikia hekta 1,200,000 za umwagiliaji. Maana yake ni kwamba hii labda inawezekana katika miaka mitano, lakini bado ina maana kwamba zitabakia hekta 27,800,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa bado naomba nitoe msisitizo kwamba hatuna budi sasa tuone mipango yetu ya Serikali tunafanyaje ili angalau tufikie hatua nzuri tuweze kujikomboa katika kilimo hasa kwa kutumia kilimo cha umwagiliaji badala ya kutegemea mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba, Serikali haina budi kuona jinsi gani tunaweza tukaboresha hii miundombinu ya umwagiliaji lakini pia uhamasishaji wa Sekta Binafsi na wadau mbalimbali waweze kushiriki katika hili suala la kilimo cha umwagiliaji ili mwisho wa siku sasa tuweze kuwa na mapinduzi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa sita wa Taarifa hii imezungumziwa kuhusu maabara ya mbegu katika Makao Makuu ya Wakala wa Mbegu za Kilimo Morogoro. Hili jambo naipongeza sana Serikali, lakini pamoja na pongezi hizo nina ushauri kwamba, Serikali ione umuhimu kwamba kuna hii maabara ya mbegu lakini kuna kila sababu ya kuwa na maabara ya kupima udongo katika maeneo mbalimbali ya nchi hii. Kama tutaweza kupima udongo, ina maana kwamba zile mbegu ambazo zitakazosiwa zitaendana na ule udongo kulingana na rutuba yake. Kwa hiyo mwisho wa siku ina maana kwamba mazao yatakayopatikana yatakuwa ni mazao ambayo yataleta tija. Kwa hiyo, naomba nitoe ushauri huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilisoma mahali nikaona kwamba, wenzetu Mkoani Kigoma walikuwa na mradi wa FAO, mradi ule ulikuwa ukiwaelekeza wakulima jinsi ya kupima afya na ubora wa ardhi. Sasa basi hebu Serikali ione itawezaje kuendesha huu mradi katika maeneo mengine ili wakulima waweze kupima ardhi na hatimaye waweze kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijatenda haki kama sitazungumzia suala la zabibu. Sisi katika Mkoa wa Dodoma zao letu ambalo ni mkombozi ni zao la zabibu, lakini katika mpango huu sijaona sehemu yoyote ambayo Serikali, imezungumzia kidogo sana katika taarifa ya kamati, lakini bado sijaona mkakati wa Serikali wa kuendeleza zao la zabibu katika Mkoa wa Dodoma. Jamani zao la zabibu ni utajiri katika Dodoma, zao la zabibu ni siasa katika Dodoma, lakini tatizo ni kwamba, zao la zabibu bado halina pembejeo. Mbegu ambazo zinatumika ni zile za miaka nenda miaka rudi kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali ione jinsi gani itakavyoweza kusaidia kukuza hili zao la zabibu ili ndugu zetu wa Mkoa wa Dodoma waweze kuondokana na suala zima la umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi wamezungumzia kuhusu suala la mafuta. Na hasa wamezungumzia jinsi gani ya kuweza kuboresha mbegu za alizeti, mbegu za mchikichi, na kadhalika. Lakini basi hebu tuone kwamba, Serikali ijaribu kuangalia zaidi; kuna mafuta ya karanga, kuna mafuta ya ufuta, kuna mafuta yanayotokana na mifugo, vyote hivi najaribu kuona ili kusudi tuweze kupunguza utegemezi wa kupata mafuta kutoka nje.

Ninakumbuka miaka ya nyuma tulikuwa tuna mafuta ya pamba. Je, kwa nini Serikali isifikirie kuona umuhimu wa kuanzisha tena zile ginnery za mafuta ya pamba, ili kusudi tuweze kupunguza upungufu wa mafuta? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nashauri sana hebu Wizara ione hilo, lakini jambo jingine kama muda utaniruhusu nilikuwa naomba nizungumzie kuhusu suala la afya. Kwenye suala la afya katika ule mpango wamezungumzia kwamba, vifo vimepungua kutoka 432 kwa vizazi hai laki moja. hadi sasa vifo vimekuwa 321,000 kwa vizazi hai laki moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kwamba, pamoja na kupunguza lakini hii namba bado ni kubwa. Tunatamani, yaani ndoto yangu natamani kama mwanamke nione wanawake hawafi kutokana na uzazi na hili jambo linawezekana. Kwamba, tukiwa na mipango kabambe ya kuhakikisha kwamba, wanawake hawa hawapotezi maisha yao tutapunguza mayatima na tutapunguza na mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba, wenzetu nchi ya Rwanda wameweza sana kujitahidi kupunguza vifo vya akinamama na watoto kwa kuwafuatilia kuona kuhakikisha kwamba, mwanamke au mama lazima kumfuatilia mpaka mwisho kuona anajifungua na anajifungua salama. Kwa hiyo, kama itawezekana na sisi tungeweza tukaweka program au kwa kufanya field visit, jinsi utakavyoiita, ili kusudi wataalamu wetu waweze kwenda kule, waweze kwenda kujifunza, kuona jinsi gani wenzetu wameweza kufanikiwa. Na naamini kabisa kujifunza ni jambo jema kabisa, mwisho wa siku na sisi inaweza ikawa vifo vya akinamama na watoto ikawa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa uchache niliona nichangie hayo. Baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, asante sana, nashukuru kwa kunipa fursa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuleta hoja yake hapa ambayo ni Mapitio na Maelekezo ya Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Bunge 2021/2022. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia kuhusiana na Mkoa wa Dodoma lakini baadaye nitazungumzia kuhusiana na suala zima la ugonjwa wa UKIMWI, madawa ya kulevya pamoja na kifua kikuu. Sisi katika Mkoa wa Dodoma kwanza tunamshukuru sana Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu na pia kuifanya kuwa Jiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna miradi mikubwa ya kimaendeleo ambayo inatakiwa itekelezwe katika Mkoa wa Dodoma ili kusudi iweze kuleta picha halisi na sura halisi ya Makao Makuu. Ipo mingi ambayo imetekelezwa, lakini nina ushauri kwamba tuna uwanja wa ndege wa Msalato, sisi wananchi wa Dodoma tunafurahia sana kuwepo uwanja huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi uwanja huu pesa zake zipo, lakini tatizo lipo kwenye fidia, kwamba wale wananchi ambao walitakiwa walipwe fidia, wako wananchi kama 1,053 kati yao waliolipwa fidia ni 874, kwa hiyo bado 176. Kwa hiyo tunaiomba Hazina iharakishe kuwalipa wananchi hawa ili kusudi mwisho wa siku kazi iweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuna waathirika ambao ni outer ring road ya Dodoma, barabara ambayo ikijengwa itaondoa sana msongamano wa magari katika Mkoa wetu wa Dodoma. Barabara hiyo ina kilometa 112 na waathirika ambao wanatakiwa kulipwa ni 2,672 ambao wanatakiwa kulipwa zaidi ya bilioni 15.7. Kwa hiyo naiomba Serikali ione umuhimu wa kuharakisha kuwalipa waathirika hawa ili kusudi kazi iweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba niikumbushe Serikali kuhusiana na barabara muhimu ambazo zitaleta maendeleo ya kiuchumi katika Mkoa wa Dodoma, barabara hizi zikijengwa kwa kipindi muafaka ina maana kwamba wananchi wa Dodoma tutafaidika Zaidi. Tunaishukuru sana Serikali kwa maendeleo yote ambayo imeifanya lakini pia tukipata barabara hizi zitatusaidia sana. Miongoni mwa barabara hizo ni pamoja na Barabara ya Mpwapwa - Gulwe - Kibakwe ambayo ina kilometa 124; Stesheni ya Gulwe - Kongwa Junction - Simanjiro hadi Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna daraja la TANESCO Mpwapwa linahitaji kufanyiwa matengenezo na daraja la Godegode ambalo limekuwa tatizo kubwa sana. Sambamba na hilo, Marehemu aliyekuwa Rais wetu pia alituahidi kwamba itajengwa bandari kavu ya kilometa sita katika eneo la Ihumwa. Kwa hiyo tunaomba Serikali ione kwamba mambo haya yanafanyika. Pia naomba nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba pale anapokuwa akitembea kuhusiana na mazao ya kimkakati, yale mazao matano, basi aone pia na zao la zabibu katika Mkoa wa Dodoma, tufanyiwe liwe zao la mkakati ili wananchi wa Dodoma waweze kuondokana na suala la umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie kuhusu masuala ya UKIMWI. Mimi ni Mwenyekiti wa Masuala ya UKIMWI kuna mambo kadhaa nilitamani kuyakumbusha, lakini niipongeze sana Serikali kwa kazi nzuri sana ambayo imeifanya ya kufanya maambukizi yaweze kupungua. Hata hivyo, naomba kutoa ushauri kwamba, kundi la vijana inabidi liangaliwe sana kwa sababu hili ndio kundi la waathirika wakubwa, Serikali iweze kuweka nguvu Zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tuna ule Mfuko wetu wa Aids Trust Fund, Serikali ione umuhimu wa kuwa na vyanzo vya kudumu vya kutunisha Mfuko huu. Jambo kubwa ambalo nataka pia niwaambie Waheshimiwa Wabunge hasa wanaume, kwa sababu takwimu imeonyesha kwamba wanaume wengi hawajitokezi kupima UKIMWI. Kwa hiyo tunaomba tuanze mfano na Wabunge wanaume humu ndani, waweze kupima UKIMWI na wakitoka hapo waweze kwenda kuhamasisha kwenye zile jamii zao kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ziara zetu tulikutana na wenye VVU, wakasema wao wanaishi kwa malengo kwa sababu wanaijua afya yao na sisi tunaoishi kwa matumaini maana yake hatujui afya zetu. Kwa hiyo natamani kwamba hebu idadi ya wanaume wajitokeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kuzungumzia ni kuhusu tohara. Kwa kweli tohara ya wanaume pia ni muhimu sana kwa sababu imeonekana kabisa inasaidia kutokuleta maambukizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia ni kuhusu madawa ya kulevya. Vijana wetu wengi sana wameathirika na madawa ya kulevya. Kwa hiyo tunaishauri Serikali ijenge Ofisi ya Kanda ili kusudi kuweza kuwahudumia hawa vijana hasa wale waraibu waweze kupata hizi dawa za methadone.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo napenda niishauri Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa masuala ya UKIMWI, kifua kikuu na dawa za kulevya watoe elimu ya lishe katika vituo vyote vya tiba na mafunzo, kwa sababu hii elimu ya lishe itawasaidia wale wenye VVU au wale wagonjwa ili kusudi afya zao ziweze kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda sio rafiki sana naomba niseme kwa uchache kwamba, kwenye magereza yetu kumekuwa kuna shida sana ya msongamano, hivyo kusababisha magonjwa ya kuambukiza hasa TB. Kwa hiyo naomba Serikali iliangalie hili jambo, tuweze kupambana na kifua kikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja na nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa ajili ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niwapongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake yote kwa kuandaa hotuba hii. Najua muda ni mfupi sana, mambo ni mengi lakini nitajitahidi kwa kadri ya uwezo wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianzia kwenye ile hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna picha pale imeonyesha kwamba kuna mmoja wa wabunifu akiwa katika kiti cha walemavu ambacho alikibuni katika sherehe za kitaifa za sayansi na teknolojia mwaka 2020. Sasa napenda kufahamu hawa watoto wetu wanaonyesha ubunifu na pengine na Watanzania wengine wengi, je, baada ya ubunifu huu nini kinaendelea, ni faida gani au tija gani inayopatikana baada ya ubunifu huu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu. Napenda kuzungumzia kuhusu suala la uendelezaji elimu ya msingi pamoja na sekondari. Katika ukurasa wa 7 wa hotuba hii Mheshimiwa Waziri amezungumzia kwamba wamepeleka walimu 174 wa shule za sekondari ambao wamejengewa uwezo wa huduma za unasihi mashuleni. Mimi naishauri Serikali, tatizo la wanafunzi wetu ni kubwa yaani wana mazonge makubwa sana, kwa hiyo, wanahitaji sana kupata watu wa kwenda kuwaambia yale mambo yanayowasibu. Kwa hiyo, hii idadi ya walimu 174 kwa kweli ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba kama ikiwezekana ingewekwa programu maalum ya kuweza kuwafundisha walimu wengi zaidi hii elimu ya umahiri katika suala zima la unasihi ili kusudi walau kila shule ya msingi, sekondari na katika vyuo wawepo walimu hawa waweze kuwasikiliza hawa watoto na vijana wetu kwa sababu tatizo hili ni kubwa sana. Ikiwezekana walimu hawa wa unasihi wawe wengi, wawe zaidi ya wawili au watatu ili mwanafunzi akiwa anahitaji huo unasihi aone ni mwalimu yupi ambaye anaona yeye mwenyewe anafaa kwenda kumpa ile shida yake aweze kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naipongeza sana Wizara kwa sababu mimi professionally ni mwalimu najua tulikotoka, hali kwa kweli imebadilika. Haya yote tunayazungumza tunaishauri tu Serikali ili kusudi kuweza kuboresha zaidi. Jamani, mimi nilikuwa mwalimu mwaka 1984 sasa nikiangalia hii trend Wizara you deserve all the best. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesema kwamba imetoa mafunzo kwa walimu 1,076 ili waweze kuwafundisha wanafunzi wasioona, wenye ulemavu wa akili na ambao wana matatizo mbalimbali ya ulemavu. Naomba nitoe ushauri kwa sababu watoto wenye mahitaji maalum wako wengi na sisi tunahamasisha sana hili suala la elimu jumuishi ni vizuri kama Serikali au Wizara ikaona kuna muhimu kuwe na basic knowledge yaani ianzie katika mitaala ya elimu ili kusudi kila mwalimu aweze kupata basic knowledge ya jinsi gani atakavyoweza ku-deal na hawa watoto wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona kabisa sasa hivi kwa mfano hii elimu ya alama, kwa kweli elimu ya alama inahitajika sana. Kwa hiyo, kama watu wakipata zile basic skills ikawekwa kabisa kwenye mtaala ikawa compulsory ingawaje kuna wengine ambao watakuja kubobea basi ni budi Wizara ikaona kwamba at least katika mitaala kukawa kuna ulazima wa kusoma masomo hayo ili kusudi walimu wote ikiwezekana wawe wana zile basic knowledge za jinsi ya ku- deal na hawa watoto wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia kuhusu suala la mitaala, wenzangu wengi sana wamezungumzia, kwa kweli sisi tunaendelea kuishauri Wizara ijaribu kuona kwamba hii mitaala irekebishwe ili kusudi iweze kuendana na mahitaji ya sasa. Tumeona kabisa kwamba nchi yetu imeingia katika uchumi wa kati na hii mitaala lazima iangaliwe upya. Tunajua kabisa kwamba kuna stadi zimewekwa kule basi ni budi sasa kuangalia stadi nyingi zaidi ili kusudi hawa watoto wetu zile stadi wazitumie kujiendeleza badala ya kusema kwamba wanategemea kazi za kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nilitamani na walimu pia ungewekwa utaratibu maalum wa refresher course za mara kwa mara. Hizi courses zitawasaidia kupata uwezo mzuri zaidi wa kuweza kuendana na hii hali halisi ya sayansi na teknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna hili suala la kisomo chenye manufaa. Nakumbuka miaka ya nyuma kulikuwa kuna utaratibu wa kisomo chenye manufaa kwamba kuna wale watu ambao hawakupata fursa ya kusoma basi kuwe kuna utaratibu kwamba ikifika wakati kuna masomo yale ya jioni, kulikuwa kuna walimu na Waratibu Elimu Kata wakifanikisha hilo. Nakumbuka kipindi cha Rais Marehemu Julius Kambarage Nyerere kuna baadhi ya wanafunzi waliokuwa bora walikuwa wanapelekwa kwenda kufundisha kwenye ile elimu ya Ngumbaro. Ili kupunguza watu wasiojua kusoma na kuandika ni budi basi Serikali ikaona kwamba inafufua vipi hiki kisomo chenye manufaa. Kwa hiyo, huo pia ulikuwa ni ushauri wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine nataka kushauri kwenye upimaji wa umahiri katika ngazi ya chekechea. Tunajua kabisa kwamba Serikali ina lengo zuri sana la kutaka kuona kwamba tunapata msingi mzuri hasa kwenye hii elimu ya chekechea. Najua kabisa katika elimu ya chekechea kuna umahiri ambao unapimwa kwa wale watoto kwa mfano, umahiri wa kutunza afya zao, kutunza mazingira, kuwasiliana, kuhusiana na kutumia zana za hisabati na kumudu stadi za kisanii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pale natamani hapa ndiyo tuweze kujua vipaji vya wale watoto wetu tunapoanzia nao kuanzia chekechea. We build up from there kwamba akipelekwa kwa yule mwalimu wake anayemfundisha darasa la kwanza akaambiwa kwamba huyu kipaji chake ni muimbaji mzuri tunaanza kumuanzishia pale. Huyu ameonesha kukaa sana na vifaa vya magari basi tumpeleke katika trend ile. Kwa hiyo, natamani Wizara au Serikali ione umuhimu sasa wa kuwaangalia hawa watoto tunawaendelezaje kutokea pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani nitoe ushauri kuhusiana na suala la hawa wanafunzi ambao pamoja na upimaji utakuta kuna wengine hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Nafahamu kwamba Wizara imeweka utaratibu kama ikitokea hivyo mtoto wa darasa la kwanza au la pili anaweza kukaririshwa lakini kama maendeleo yake bado duni tunafanyaje? Ni vizuri sasa tuweke utaratibu au kuweka madarasa maalum ili kuweza kuwasaidia hawa watoto ambao wana uwezo duni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda ni mfupi sana naomba niunge mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Najua muda ni mchache sana lakini nitajitahidi. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa maandalizi ya bajeti hii, lakini sambamba na hilo naomba nitoe ushauri kwamba, pamoja na kwamba Serikali imeweka vipaumbee vyake katika Fungu la 52 pamoja na Fungu 53, naomba nitoe ushauri ufuatao:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la kuimarisha huduma ya chanjo, naomba niishauri Serikali kwenye hii issue ya chanjo ya ugonjwa wa ini ni kwamba chanjo hii ili ukitaka kuchanja inabidi utoe shilingi 20,000 pale unapokwenda kupima halafu baadaye inabidi utoe Shilingi 10,000, Shilingi 10,000, Shilingi 10,000 kwa ajili ya dozi. Naomba Serikali ione ili kusudi wale wananchi wa pembezoni waweze kuweza kuchanja chanjo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka nizungumzie kuhusiana na wanawake ambao wanakwenda kujifungua. Taarifa zinaonesha kwamba imeonekana kwamba wanawake wengi wanajitahidi kwenda kujifungulia kwenye kliniki na hospitali, lakini bado kuna wale wachache ambao bado wanajifungua kwa waganga au wakunga wa jadi. Nashauri elimu iendelee ili kusudi watoto wawe salama na akinamama wawe salama, ni vizuri wakaenda kujifungulia katika hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda nizungumzie suala la magonjwa ya kuambukiza ikiwemo Malaria, Kifua Kikuu na hasa UKIMWI nijikite zaidi kwenye UKIMWI.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi sana wamezungumzia kuhusu hili suala la UKIMWI na inaonyesha kabisa kwamba kundi kubwa ambalo liko kwenye hatari ya kuambukizwa UKIMWI ni hawa Watoto kuanzia miaka 14 mpaka 24. Takwimu zinaonyesha kwa mfano katika Mkoa wa Njombe kwamba maambukizi yako kwa asilimia kama 11.3 kwamba hawa Watoto wenye umri kati ya miaka hiyo 14 na 24 katika wale vijana 10 wanaopimwa wa kike wanaonekana kwamba wanamaambukizi makubwa sana. Kwa hiyo, ina maana kwamba Watoto wa kike 8wanapata maambukizi katika 10. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri akinababa hebu muwaonee huruma hawa Watoto, kwasababu inaonekana kwamba mmeacha kwenda kwa akinamama watu wazima mnawafuata hawa Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa wale wa baba ambao wanakwenda kuwadanganya hawa Watoto hebu waacheni hawa Watoto hebu waacheni hawa Watoto wasome wafikie malengo yao. Kwa hiyo nilikuwa naomba nishauri. Lakini sambamba na hilo wenzangu wamezungumza kuhusiana na suala zima la kwenda kupima UKIMWI tunaendelea kuhamasisha wanaume waende wakapime Ukimwi kwasababu kama hawa Watoto wa kike wadogo wanakuwa hawana maambukizi haya maambukizi mapya wanayapata wapi? Ina maana kwamba wanayapata kwa wale akina baba ambao hawajapima Ukimwi. Kwa hiyo nilikuwa naomba nishauri kwamba akina baba bado waendelee kujitokeza kupima Ukimwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo jingine nililokuwa nataka kuzungumzia ni kuhusiana na huduma za uzazi wa mpango. Ni kwamba inaonyesha kwamba katika hotuba imeonyesha kwamba katika hotuba inaonyesha kwamba kuanzia Julai 2020 hadi Machi, 2021 inaonesha takwimu za akinamama ambao wamepata uzazi wa mpango ni 4,926,183 kati ya akinamama 13,841,830 sawa na asilimia 36. Hii bado ni asilimia ndogo kwa hiyo nilikuwa naiomba Serikali pia iwekeze sana kwenye suala zima la uzazi wa mpango ili kusudi tuweze kupanga mipango yetu ya maendeleo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilikuwa naomba nizungumzie kuhusiana na huu mpango kazi wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na Watoto MTAKUWA wa mwaka 2017 hadi 2018, 2021/2022. Najua azma nzuri sana ya Serikali kwa ajili ya mpango huu nikuhakikisha kwamba ukatili unapungua au unakwisha kabisa. Lakini tatizo linakuja kwamba hivi vikundi vya MTAKUWA katika ngazi ya vijiji na kata havipati pesa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali ione Wizara ya Afya pamoja na TAMISEMI washirikiane kuona kwamba zinapangwa bajeti ili kusudi huku katika ngazi za vijiji na kata vikao hivi viweze kukutana kuweza kufanya mikutano yao ili kupinga suala zima la ukatili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda siyo Rafiki…

NAIBU SPIKA: Imeshagonga kengele Mheshimiwa.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nami nashukuru kwa kunipa fursa niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kuandaa hotuba hii. Najua muda ni mchache sana lakini nitajitahidi.

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu kuipongeza sana Serikali, kwa kuifanya sekta ya kilimo iweze kutoa mchango mkubwa sana katika ukuaji wa kilimo, wa uchumi, lakini sambamba na hilo katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba, kilimo kimechangia asilimia 65 ya malighafi za viwanda niipongeze sana Wizara kwa kufikia hatua hii.

Mheshimiwa Spika, sambamba na pongezi hizo naomba nitoe ushauri kwamba, iwapo bajeti itakuwa ya kutosha ina maana kwamba, uwezekano wa uchumi wetu kukua kutokana na kilimo unaweza ukafika zaidi ya asilimia 90. Lakini sambamba na hilo, hata katika upatikanaji wa malighafi ikipatikana pesa ya kutosha kwamba, kilimo kikawa kina tija ina maana kwamba, uchangiaji katika zile malighafi unaweza ukafika asilimia 100 na hatimaye mwisho wa siku, tunaweza tukapata ziada zaidi na tukaweza kuuza nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kubwa ninachoweza kuishauri Serikali hapa ni kwamba, kuona jinsi gani tunaweza kupata bajeti ya kutosha ili kusudi kuweza kuwekeza katika kilimo. Naomba pia, nizungumzie kuhusu kilimo cha umwagiliaji, wenzangu wengi sana wamezungumzia kuhusu kilimo cha umwagiliaji. Niipongeze sana Serikali kwa kuweza kuwa na hekta 694,715 kwa mwezi Mei, 2020 hadi hekta 695,045 mwezi Machi, 2021 hii iko katika ukurasa wa 10 wa hotuba hii. Kumbe ni kwamba tukiwekeza zaidi katika kilimo tija itakayopatikana ni kubwa sana na sasa kubwa ni kwamba, Wizara ione umuhimu wa kuhamasisha wananchi waweze kujikita zaidi kwenye kilimo cha umwagiliaji kulikoni kilimo cha mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo kwamba, wadau wengi zaidi waweze kuingia katika kilimo cha umwagiliaji. Naamini kabisa mapinduzi ya kilimo yanaweza yakawezekana na hatimaye, sisi tukawa ni miongoni mwa nchi ambayo inaweza ikalisha hata nchi mbalimbali katika dunia hii. Lakini pia mazao ya biashara yanaweza yakapatikana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nilitaka kuzungumzia ilikuwa ni kuhusu bima ya kilimo, niipongeze sana Serikali kwa kuona umuhimu wa bima ya kilimo. Ninajua kabisa kwamba bima hii kutokana na taarifa ambayo nimeiona katika hotuba hii, inaweza ikasaidia wananchi wengi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu mkubwa ni kwamba, Serikali sasa iharakishe kukamilisha ule Mpango wa Taifa wa bima, kwa ajili ya kilimo ili kusudi kuwanusuru wananchi wengi zaidi. Na wakulima wengi Zaidi, waweze kuelimishwa kuhusu hii bima ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo natamani kulizungumzia ni zao la zabibu. Kwanza niipongeze sana Serikali kwamba katika hotuba hii, ukiangalia ukurasa wa 27, ukurasa wa 107, ukurasa wa 131 na ukurasa wa 158, kuna element ya zabibu imezungumziwa pale. Kwa hiyo, hapa sasa tunaona mwanga kwamba sasa Serikali inaona kwamba, kuna umuhimu wa kuwekeza katika hili zao la zabibu, lakini sambamba na hilo nilikuwa naomba niishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mashamba katika maeneo mbalimbali mfano katika Wilaya ya Chamwino kuna shamba, kuna maeneo ya Gawaye kuna shamba, kuna eneo la Hombolo kuna shamba na kuna baadhi ya maeneo ya Bahi na kadhalika. Ushauri wangu, Serikali ingeona umuhimu wa kuweza kufanya block farming katika zabibu na ikiwezekana zabibu nayo iwe ni zao la kimkakati katika Mkoa wa Dodoma. Kwa sababu, unapozungumzia zabibu, zabibu katika Dodoma ni siasa, zabibu katika Dodoma ni uchumi. Kwa hiyo, ushauri wangu ulikuwa ni huo, Serikali ijaribu kuwekeza zaidi na zaidi katika zao la kilimo kwa sababu, sisi wana Dodoma tunaona kabisa kwamba, zabibu ni fahari ya Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ninasema hivyo kwasababu kwamba zabibu ya Dodoma yenyewe ni unique sana. Kwasababu imekuwa ikizaliwa kwa vipindi viwili, yaani kwa awamu mbili unaweza ukapata zabibu na hii ni very unique. Kwa hiyo, ninachosisitiza ni kwamba, Serikali ione umuhimu wa kulifanya kwamba zao la zabibu liwe ni zao la kimkakati katika Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia niwapongeze sana Wizara kwamba, katika ukurasa wa 89 wa hotuba ya Waziri, amezungumzia hatua ambayo Wizara imekuwa ikichukua, kutoa huduma ya lishe kwa wale wafanyakazi ambao wameonekana na VVU hongera sana kwa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri Wizara zingine, Idara za Serikali na Taasisi za Serikali, zione umuhimu pia wa kuona kwamba, wale wafanyakazi wote ambao wamejidhihirisha na wale ambao hawakujidhihirisha, tunawashauri kwamba wadhihirike, ili kusudi waweze kupata huduma ya lishe kwa ajili ya watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizungumzie kuhusu mazao ya bustani, mazao ya bustani bado bei ya zile mbegu ni kubwa na mbegu zinatoka nje. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kushauri kwamba ikiwezekana basi, hebu hizi taasisi zetu za ndani nazo ziweze kuzalisha mazao bustani, kama vile mbegu za nyanya, mbegu za matikiti na nyinginezo ili kusudi sasa, zikiuzwa hapa ndani kwa bei ya ndani itakuwa ni bei nafuu Zaidi, kulikoni ambayo ile inayotoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa fursa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema. Sambamba na hilo naomba nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kuandaa hotuba hii. Pia naomba niwapongeze Wizara pamoja na bajeti finyu, lakini kuna mambo ambayo tunayaona yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri, naomba niipongeze Serikali kwamba asilimia 17 ya Pato la Taifa linatokana na utalii. Sambamba na hilo, asilimia 25 ya pesa za kigeni zinatokana na utalii. Pia Sekta ya Utalii imeweza kuzalisha ajira 1,600,00, jamani hili sio dogo, lazima tuipongeze sana Wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie zaidi kuhusiana na kutangaza vivutio vya utalii hasa kupitia vyombo vya habari. Ni ukweli usiopingika kwamba vyombo vya habari ni nguzo kubwa sana katika kusaidia kutangaza vivutio katika nchi yetu ili watalii wengi zaidi waweze kufika katika eneo letu. Pia vyombo vya habari ni tegemeo muhimu sana katika kukuza utalii katika nchi yetu.

Sambamba na hilo, natambua kwamba Wizara imekuwa ikijitahidi sana, lakini naomba nishauri na ushauri wangu unatokana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 31 hadi 33 amebainisha kwamba Wizara imeandaa vipindi 70 vya television, vipindi 51 vya redio na makala 36 kuhusu uhifadhi na vivutio vya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi hizo, naomba niishauri Wizara kwamba, ufike wakati sasa waandae mpango mkakati kwa ajili ya Waandishi wa Habari kutangaza vivutio vya utalii Tanzania. Kama watasema labda Media Strategy for Tourism in Tanzania ili sasa ule mpango mkakati uweze kutumika kwa ajili ya kuandaa Waandishi wa Habari mbalimbali waweze kuandika habari za utalii kwamba wawe wame-specialize katika kuandika habari za utalii. Naamini kabisa kwa kuandika habari nyingi zaidi za utalii pamoja na mengi yanayofanyika, tunaona kabisa kwamba kuna electronic media imekuwa ikijitahidi, lakini basi hebu uwekwe mkazo kuwe kuna ile media strategy ili kusudi mwisho wa siku sasa katika ile strategy ambayo itakuwa inaelezea malengo, ione jinsi gani ya utekelezaji na pia iwepo bajeti maalum kwa ajili ya Waandishi wa Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kabisa kwamba wasanii wamekuwa engaged kwa njia moja au nyingine, sasa hebu tuone kwamba engagement ya media nayo iwe katika mtindo wake ili kusudi sasa Waandishi wa Habari waweze kuandika vizuri hizi habari za kuhusu utalii. Nafahamu kwamba kwa mfano Mashirika kama TANAPA, Ngorongoro, TFS na TAWA yamekuwa yakishirikiana na Waandishi wa Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina uhakika kama Wizara ina mpango maalum mkakati wa kuwashirikisha Waandishi wa Habari kwa muda wote, yaani isiwe tu kwamba kwa matukio fulani au labda ndani ya mwaka no, yaani kiwe ni kitu ambacho ni endelevu. Naamini kabisa Waandishi wa Habari wakishirikishwa kwa kipindi hiki wanaweza wakaleta mafanikio makubwa sana katika kuleta tija katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Waandishi hawa wa Habari, kukiwa kuna ile media strategy lakini pia waende wakajifunze katika zile nchi ambazo zimefanikiwa zaidi katika kuvutia watalii. Kwa mfano katika Afrika wenzetu kama Misri, South Afrika, Zimbabwe, Zambia na wengineo, wameweza sana ku-advertise. Pia kuna nchi zingine za nje kwa mfano kama Ufaransa, Italia, United States, Spain wao pia wameweza sana ku-attract watalii wengi sana. Kwa hiyo nashauri kwamba ufike wakati sasa na sisi tuwe tuna Waandishi wa Habari maalum kuhusu masuala ya utalii katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda siyo rafiki sana, basi kwa uchache, naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. FATMA H. TOUFIQ – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MASUALA YA UKIMWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge waliochangia katika Taarifa yetu ya Kamati ya Masuala ya UKIMWI kwa mwaka 2021/ 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia ni saba, lakini pia upande wa Serikali tumepata ufafanuzi kutoka kwa Mawaziri wawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wabunge waliochangia, naomba kwanza nianzie upande wa Serikali ambapo Naibu Waziri wetu Mheshimiwa Ummy Nderiananga, ameipongeza sana Kamati na amekubali kwamba ushauri wote ambao Kamati tumeutoa utachukuliwa na utakwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba kwa niaba ya Kamati niendelee kuipongeza sana Serikali na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwa kinara wa kuhamasisha wanaume kwenda kupima. Naamini kabisa, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kinara, basi wanaume wengi zaidi watajitokeza na jamii kwa ujumla watakwenda kupima ili kusudi tuweze kupunguza hili suala zima la maambukizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Naibu Waziri amezungumzia kuhusu programs za vijana, tunashukuru sana. Basi nasi tunaendelea kusisitiza program hizi ziendelee ili kusudi tuweze kuwanusuru vijana wetu, kwa sababu tumeona kwamba kundi ambalo limeonesha kabisa kwamba linaathirika kwa sana ni la vijana kati ya miaka 15 – 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu amezungumzia kuhusu suala zima la elimu hasa kwa Community Health Workers kuhusu magonjwa yasiyo ambukiza. Tunashukuru sana kulichukua hilo, tunaamini kabisa yote yatafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, amezungumzia kwamba uratibu umeshaanza chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa hiyo, hili nalo sisi kama Kamati tunaendelea kuishauri Serikali ione namna bora kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu i-take lead kwa sababu hili jambo ni suala mtambuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba niendelee kuipongeza sana Serikali hasa kwenye hili suala la magonjwa yasiyoambukiza kwa sababu kumekuwa na political will, tumeona kabisa jinsi gani Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amekuwa akiongoza matembezi ili kuhakikisha kwamba Watanzania tunaendelea kuwa afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tumeona Mheshimiwa Makamu wa Rais akiongoza matembezi na Mheshimiwa Waziri Mkuu; yote haya inaonesha kabisa kwamba Serikali ina nia ya dhati kabisa kuhakikisha kwamba suala zima la magonjwa yasiyoambukiza nchini kama siyo kupungua basi linakwisha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende kwa Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia hoja hii. Jumla ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia ni saba, akiwemo Mheshimiwa Abdul-Hafar, Mheshimiwa Neema Mwandabila, Mheshimiwa Tecla Ungele, Mheshimiwa Dkt. Chaya, Mheshimiwa Dkt. Alice, Mheshimiwa Dkt. Nyamoga na Mheshimiwa Mama Mushashu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ushauri wao, tumegundua kwamba jambo kubwa ambalo limezungumziwa hasa kwenye suala zima la Ukimwi, ni kuhusu Aids Trust Fund. Miongoni mwa ushauri ni kwamba hii kuwe kuna chanzo mahususi cha kutunisha mfuko huu. Naamini kwamba hili Serikali watakuwa wamelipokea, kwa sababu tunatamani hili suala la afua ya Ukimwi, fedha zitokane na sisi kwa fedha zetu za ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye suala zima la elimu ya Ukimwi ni kuhusu matumizi ya condom. Mheshimiwa Abdul-Hafar amesisitiza suala la matumizi ya condom na pia kuhabarisha vijana wetu ili kusudi wasiende kuianza ngono mapema, lakini kama ikibidi, basi waweze kutumia zile njia za kujizuia ili mwisho wa siku wasiweze kupata maambukizi mapya.

Meshimiwa Spika, jambo lingine ambalo limezungumziwa ni kuwepo na Tume itakayoshughulikia maradhi yasiyoambukiza. Hapa Waheshimiwa Wabunge watatu wamelizungumzia hili, nami kama Mwenyekiti wa Kamati pamoja na Kamati yetu, katika taarifa yetu, maoni na ushauri pia tumelizungumzia hili kwamba, kama ikiwezekana, basi tunaishauri Serikali iundwe tume maalum ya kuweza kushughulika na masuala ya magonjwa yasiyoambukiza; na ikiwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, itakuwa ni nzuri zaidi kwa sababu hili ni jambo linahusu masuala mtambuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine uliotolewa kwenye issue ya elimu ya magonjwa yasiyoambukiza ni kwamba lazima kuwepo na suala la elimu ili watu waweze kujua, waweze kuchukua tahadhari mapema na kuweza kujinusuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla Waheshimiwa Wabunge wote wameongelea kuhusiana na suala zima la elimu ili kusudi wananchi au jamii iweze kuchukua tahadhari mapema wasiweze kupata magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limetolewa ushauri ni kuhusiana na wataalam wa physiotherapy. Mheshimiwa aliyetoa ushauri huu ni Mheshimiwa Nyamoga, kwamba wataalam hawa inabidi waende hadi katika ngazi ya Wilaya na ikiwezekana Serikali ione umuhimu sasa wa kujenga vyuo vya kutosha vya physiotherapy kwa sababu inaonesha kabisa kwamba magonjwa ya kuambukiza yanaongezeka. Kwa hiyo, hii itasaidia kukidhi magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limezungumziwa ni kubadili mtindo wa maisha. Kwamba ili kuweza kukabiliana na suala zima magonjwa yasiyoambukiza, tuweze kubadilisha mtindo wetu wa maisha ili mwisho wa siku tuweze kuyazuia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumziwa ni kuhusiana na madawa ya kulevya, ambapo imezungumziwa kuhusiana na waraibu kwamba itakuwa ni vizuri waweze kupatiwa miradi. Kwamba, kuna vituo ambavyo vimekuwa vikitoa hii huduma ya methadone na kuna waraibu wengine ambao wamekuwa wakipona kabisa. Sasa je, baada ya kupona wanakwenda wapi? Basi, Serikali ione umuhimu sasa wa kutafuta miradi midogo midogo kama ikiwezekana kuwapa mikopo na kadhalika hao waraibu ili kusudi waweze kurudi katika maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, suala la lishe limeonekana kwamba nalo pia ni muhimu ili mwisho wa siku hawa vijana wanaotumia methadone waweze kupata lishe ambayo ni bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Haya yote naamini kabisa kwamba Serikali itayachukua na kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa naliomba Bunge lako Tukufu kuunga mkono hoja yetu ya Kamati ya Masuala ya Ukimwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hili niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Pia naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri pamoja na wataalam wote walioandaa hotuba hii. Hali kadhalika, nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ya kutuletea maendeleo Watanzania. Mwenye macho aambiwi tazama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuzungumzia kuhusu mfumuko wa bei ambayo ipo ukurasa wa 17 na upandaji wa bei katika hotuba hii, ambayo ipo katika ukurasa wa 82. Ni ukweli usiopingika kuwa bidhaa nyingi zimepanda bei kutokana na masuala mbalimbali, lakini baadhi ya wafanyabiashara hupandisha bidhaa hizo bila kufuata utaratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuzungumzia upandaji wa vifaa vya ujenzi ikiwemo bidhaa ya nondo. Awali nondo milimita 12 ilikuwa ikiuzwa kati ya shilingi 16,000 mpaka shilingi 17,000, lakini sasa hivi nondo hiyo imeshapanda na kuuzwa kati ya shilingi 27,000 hadi shilingi 28,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali yangu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuna chuma chetu kule eneo la Liganga, sasa ili kuweza kupata bidhaa hii kama malighafi yetu wenyewe, ni budi Serikali ikaweka utaratibu au mkakati mzuri wa kuhakikisha kwamba chuma chetu cha Liganga kinapatikana kwa wingi ili kusudi tuweze kupata malighafi ambayo itapunguza baadhi ya bei ikiwemo na bei ya nondo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 10 wa hotuba hii, Waziri Mkuu amezungumzia kuhusu ujenzi wa madaraja makubwa na ujenzi wa barabara. Niendelee kuipongeza Serikali, lakini sisi wana-Dodoma tuna kila sababu ya kuishukuru sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mambo makubwa ambayo tumefanyiwa sisi katika suala zima la miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na shukurani hii, naiomba Serikali yetu sikivu itusaidie katika ujenzi wa daraja la Godegode. Daraja hili kwa kweli limekuwa ni kero sana wananchi wa Wilaya ya Mpwapwa. Kwa kweli pindi inapofikia mvua, daraja hili mawasiliano yanakatika kabisa. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu Tukufu, hili daraja la Godegode hebu lipewe kipaumbele ili tuwanusuru hawa wananchi wa Mpwapwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuna korongo kubwa ambalo linaendelea katika Mji wa Mpwapwa, nalo pia limekuwa ni hatari kwa maisha ya wananchi wa pale Mpwapwa. Basi naomba hatua za haraka zichukuliwe ili kusudi tuweze kukinga badala ya kutokea madhara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, aliweza kuzindua barabara ya mzunguko tarehe 9/2/2022 yenye kilomita 112.3 na hatimaye ujenzi ule umeanza. Sisi wana-Dodoma kwa kweli tunampongeza sana; na kwa niaba ya wananchi wa Dodoma naomba niendelee kumpongeza sana Rais wetu kwa sababu hii inaendelea kuifanya sura ya Makao Makuu iweze kuonekana katika Mkoa wetu wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilete ombi kwa Serikali kwamba kuna upembuzi yakinifu na usanifu wa barabara ya Arusha - Kibaya - Kongwa, lakini mradi huu haujatangazwa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba, kwa kuwa Dodoma ni Makao Makuu na fursa ni nyingi sana na tunatamani Dodoma ifunguke kweli kweli, natoa ushauri kwa Serikali, itakapotangaza mradi huu wa hii barabara, basi ujenzi huu uanzie kutokea Wilaya ya Kongwa na hatimaye iweze kwenda Kibaya hadi Arusha. Naamini kwa ombi hili Serikali italichukulia uzito wa pekee ili kusudi sisi wananchi wa Dodoma iweze kutufungulia maeneo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa TARURA una barabara ambayo ni kiungo kikubwa kati ya Kondoa - Tumberu na Thawe. Barabara hii nayo inahitaji sana kutengenezwa kwani inatakiwa ipitike kipindi chote, lakini wananchi wa maeneo hayo wamekuwa wakipata adha kubwa sana kwa sababu barabara hii bado ina shida. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kama itawezekana, basi Serikali nayo ione kwamba sisi wana-Dodoma tunaleta special request ili kusudi iweze kupatikana pesa iweze kujenga barabara hii ili wananchi wa Dodoma waweze kupata urahisi wa kusafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba nikumbushe ujenzi wa barabara ya Ihumwa – Hombolo, Ihumwa – Stesheni SGR. Hii ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Marehemu Rais Dkt. John Pombe Magufuli, basi tunaiomba Serikali iendelee kutusaidia kutekeleza mradi huu katika bajeti hii kama itawezekana ili tuendelee kuifungulia Dodoma kwa suala zima la usafiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijatenda haki kama nisipo zungumzia kuhusu suala zima la zabibu, kwa sababu zabibu ni nembo ya Dodoma, zabibu ni biashara Dodoma, zabibu ni siasa Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo, bado zao la zabibu lina wazalishaji. Wananchi wanaozalisha wapo, lakini tatizo ni kwamba hakuna soko la uhakika la zabibu. Kwa hiyo, nilikuwa naikumbusha Serikali ione namna bora ya kusimamia mkataba wa kilimo wa zao la zabibu ili kusudi tuweze kupata uhakika wa soko kupitia TBL ambayo ni kampuni tanzu ya TBL.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu waraibu ambayo pia ameizungumzia Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake. Kwanza niendelee kuipongeza Serikali kwa kuanzisha kliniki zinazohudumia waraibu wa dawa za kulevya, maarufu tumekuwa tunawaita mateja, lakini hilo siyo jina zuri, lakini wale ni wagonjwa, kwa sababu wana tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia program ya kukuza ujuzi na kutoa mafunzo kwa waraibu 200, hii ni hatua kubwa sana kwa sababu Serikali inaona umuhimu wa hawa watu na hawa ni binadamu na wana haki zote kama binadamu yeyote yule katika nchi yetu hii. Kwa hiyo, naishauri Serikali kwamba kupitia program hii, ni vizuri hawa waraibu wakapata mikopo ya Halmashauri 4, 4, 2; yaani wale waraibu ambao wameshapata dawa, wamepitia methadone, wameweza kupona na wamekuwa katika hali ya kawaida, basi Serikali ione jinsi gani ya kuwaingiza katika program mbalimbali waweze kupata mikopo na fursa mbalimbali ili mwisho wa siku waweze kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya maeneo tumeenda tumewakuta hawa vijana ambao wameacha kutumia madawa ya kulevya na wameanzisha familia zao; na wamekuwa ni raia wema kabisa, lakini hawana miradi ya kufanya. Kwa hiyo, naiomba Serikali ione namna ya kuwabaini na kuweza kuwasiadia ili mwisho wa siku waweze kurudi katika mazingira yao ya kawaida, kwa sababu hawa vijana wengine wanaingia kwenye uraibu kwa sababu ya kukosa kazi au kukosa shughuli ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuhusu hawa waraibu, wale ambao wamezidi miaka 15, tunaona kabisa kwamba kama ni kundi la vijana, wao wana fursa; wanawake wana fursa, vijana wana fursa, lakini wale waraibu wanaume ambao wana zaidi ya miaka 35, bado naomba Serikali ione namna bora ya kuweza kuwasaidia ili kusudi na wao waweze kufaidi hizi fursa ambazo ziko hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, niliomba pia nizungumzie kuhusiana na suala la UKIMWI; hasa nilipenda kuzungumzia kuhusu tohara ya kitabibu. Inaonyesha kabisa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Mwaka 2022/2023 kwa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote kwa kuandaa bajeti hii. Sambamba na hilo, naomba niendelee kuipongeza Serikali yangu Tukufu chini ya uongozi wa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa mageuzi makubwa sana katika elimu pamoja na ufinyu wa bajeti, lakini kazi inaonekana, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 76 wa hotuba hii, Wizara imebainisha kwamba ina dhamira ya dhati ya kuongeza fursa na ubora wa elimu ya awali, elimu ya msingi na elimu ya Sekondari, naipongeza sana. Ushauri wangu kwa Wizara, nilikuwa naomba Wizara ione umuhimu wa kuifanya Kurugenzi ya Elimu ya awali iwe peke yake ili kusudi kuipa nguvu ya usimamizi wa karibu na iwe na bajeti ya peke yake. Kwa sababu elimu ya awali ndio msingi ambapo mwanafunzi akitoka elimu ya awali, akienda katika elimu ya msingi atakuwa ameandaliwa vyema, hivyo tutakosa wale wanafunzi wasiojua kusoma na kuandika, maana yake elimu yetu itakuwa bora sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba niishauri Serikali ione umuhimu wa kuwa na kurugenzi maalum ambayo itashughulikia elimu ya awali badala ya Kurugenzi kuwa na Elimu ya Awali, Elimu ya Sekondari, Elimu na Msingi na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nizungumzie kuhusu uhaba wa watumishi wakiwemo walimu na wakufunzi; imezungumzwa lakini pia Kamati ya kudumu ya Huduma za Jamii pia imezungumzia hili jambo. Ushauri wangu ni kwamba ili kuwapunguzia walimu mzigo, kuna baadhi ya maeneo ambapo walimu wanafundisha zaidi ya wanafunzi 100, mwalimu mmoja, lakini ratio tunajua kabisa kwamba elimu ya msingi ni wanafunzi 45 na Sekondari ni 40. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba hebu Wizara iangalie upya ile ikama, kwamba katika yale baadhi ya maeneo ambayo walimu wamezidi, basi waweze kuwa-regulate ili mwisho wa siku tuweze kupunguza hili suala la mzigo kwa baadhi ya walimu kufundisha wanafunzi wengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo katika ukurasa wa 33 wa hotuba hii umezungumzia kuhusiana na udhibiti ubora wa shule pamoja na Vyuo vya Ualimu, pamoja na Serikali kuhakikisha kwamba Elimu ya Awali Msingi na Sekondari na Walimu inafuata kanuni na miongozo iliyopo. Nina ushauri kuhusiana na udhibiti ubora wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika taarifa ya Kamati imeonesha kwamba fedha kiasi cha Shilingi bilioni moja kwa ajili ya ukaguzi kwa mwaka 2021/2022 hazikutolewa. Kwa hiyo, naiomba Serikali na Wizara kwa ujumla, hebu watoe fedha hizi, kwa kweli wakaguzi tunahitaji kuwawezesha kifedha ili kusudi waweze kukagua hizi shule zetu na waweze kutoa ushauri ili mwisho wa siku ule upungufu utakaoonekana uweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali itoe fedha kwa sababu kuna baadhi ya maeneo katika Halmashauri, magari yale ya ukaguzi yamelala kwa sababu hakuna fedha za kuziendeshea, lakini pia kuna baadhi ya maeneo kutoka Halmashauri ya Wilaya ni mbali na Makao Makuu, kwa hiyo, wanapokwenda kukagua, sometimes wanakuwa hawana fedha. Kwa hiyo, zile fedha zikija kwa wakati, ina maana kwamba wakaguzi hawa watatimiza malengo yao na hatimaye ufanisi wa elimu utatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilikuwa nataka kuzungumzia ni kuhusu miundombinu ambayo ni pamoja na vyumba vya madarasa, nyumba za walimu, maabara, mabweni, madawati, meza za walimu pamoja na maktaba. Natambua juhudi za Serikali, lakini bado kuna upungufu. Hata hivyo, tuendelee kuwapongeza baadhi ya wadau zikiwemo benki mbalimbali ambazo zimekuwa ziki- support katika masuala mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa nilitamani nizungumzie kuhusu maktaba. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, amezungumzia kabisa kwamba katika ukurasa wa 26 amezungumzia kuhusiana na suala la Maktaba na kwamba katika shule wameweza kutenga Maktaba 171.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri kuhusiana na suala zima la maktaba. Maktaba zilizokuwepo katika Shule za Msingi na Sekondari zitawasaidia hawa watoto kuweza kujifunza mambo mengi. Takwimu au taarifa mbalimbali zinaonesha kwamba miongoni mwa watu ambao ni wavivu wa kusoma, Watanzania ni miongoni mwao. Ni kwamba Watanzania wengi wanapenda waende wakaangalie gazeti, zile headings tu za pale juu na yale magazeti ya udaku, lakini vile vitabu ambavyo vinaweza vikamwongezea maarifa na taarifa ambapo vinaweza vikapatikana katika maktaba, inabidi tuwandae watoto wetu mapema ili kusudi waanze kuwa na utamaduni huo waweze kujisomea na hatimaye iweze kuwaongea maarifa na taarifa. (Makofi)

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu kumpa taarifa mchangiaji ya kwamba, mchango wa magazeti ya udaku kwa Taifa hili ni mkubwa. Magazeti ya udaku siyo tu yanaandika habari za ovyo, yana habari za elimu na afya ambazo zinaweza zikamsaidia mtoto kujifunza. Kwa hiyo, naomba asijaribu tu kushusha hadhi ya magazeti haya kwa sabau yametoa mchango mkubwa kwa Taifa letu. Ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Toufiq, taarifa.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niendelee. Sikuwa na nia ya kuyadhalilisha magazeti haya, badala yake tunachotaka wanafunzi wajifunze kwenye vitabu mbalimbali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Afya kwa Mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Afya na Taasisi zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo naomba pia na mimi nichukue fursa hii kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri sana anayoifanya katika suala zima la kuleta maendeleo. Pia kuhakikisha kwamba anaiangalia sekta hii ya Afya kwa jicho la kipekee, nampongeza sana Mheshimiwa Rais. Tunajua kabisa azma yake ni kuhakikisha kwamba afya ya watanzania ina imarika ili kusudi waweze kufanya maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa Saba wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ambapo ameeleza kwamba azma ya Serikali ni kuboresha utoaji huduma pamoja na kuimarisha miundombinu ya kutolea huduma za afya katika hospitali za rufaa, hospitali za mikoa, hospitali za kanda, maalum na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili naomba nitoe ushauri, natambua kazi nzuri sana ambayo inafanywa na Serikali. Lakini pia napenda kuishauri Serikali hasa kwa Mkoa wangu wa Dodoma, katika Mkoa wa Dodoma, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, hospitali hii ni tegemeo kubwa sana kwa wananchi wa Dodoma na maeneo mengine ya Jirani.

Mheshimiwa Spika, wananchi wengi wanategemea kupata matibabu katika eneo hili. Naipongeza sana Serikali imejitahidi sana kuwekeza miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa jengo la wagonjwa la ICU lakini pia usimikaji wa mashine ya CT – Scan ambayo iko katika hospitali ile na inatumika vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hayo ni kwamba hospitali ile ina majengo mengi sana ambayo ni chakavu na ambayo yalikuwepo tangu enzi za mkoloni. Pamoja na kwamba kuna majengo ambayo yamekuwa yakijengwa lakini bado eneo lile ni dogo. Kwa hiyo, nilikuwa naomba nitoe ushauri kwamba, hebu Serikali ione umuhimu basi katika eneo lile dogo iweze kujenga majengo ya ghorofa ili kusudi kuweza kupata majengo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mpango wa Serikali wa kujenga ghorofa ambalo lingeweza kuhudumia magonjwa ya mifupa. Ushauri ni kwamba Serikali ione uharaka sasa wa kujenga jengo hili la mifupa ili kusudi wananchi waweze kupata tiba vizuri na jengo liwe la kisasa. Naamini kabisa kama likijengwa jengo hili basi huduma zitapatikana kwa uzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwamba hospitali hii ya mkoa ambayo ni maarufu kwa jina la General Hospital inapakana na eneo la jeshi ambalo liko Jeshi la polisi pale. Kwa hiyo, kuna eneo liko pale, Serikali iome umuhimu wa kulitoa lile eneo la Polisi kwa hospitali ili kusudi waweze kujenga miundombinu zaidi katika kuendeleza majengo mapya kwa ajili ya utoaji wa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine ni kuhusiana na manunuzi ya dawa katika vituo vya kutolea huduma. Kuna fedha kwa ajili ya manunuzi ya bidhaa za dawa moja kwa moja kutoka bohari, hili ni jambo jema sana. Lakini kuna nyakati bidhaa hizi yaani dawa zinakuwa hazipatikani katika bohari ya dawa. Ushauri wangu, je, Serikali haioni umuhimu wa kuwa na asilimia fulani ya fedha zipelekwe kwenye akaunti za vituo husika ili bidhaa zinunuliwe kutumia wazabuni wengine? Hii itachangia upatikanaji wa dawa pale ambapo bohari kuu inakuwa imeishiwa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niliona kwamba nishauri hili kwa sababu tumekuwa tukipata malalamiko ya mara kwa mara kuhusiana na upungufu wa dawa katika vituo pamoja na hospitali. Kwa hiyo basi, ushauri wangu kama Serikali itaona hii inafaa basi hebu ichukue ushauri huo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitamani kuzungumzia nilitaka kuzungumzia kuhusiana na suala zima la mwitikio wa UKIMWI. Natambua juhudi kubwa sana ambazo Serikali imekuwa ikizifanya kwa ajili ya kupambana na UKIMWI, naipongeza sana Serikali. Hata hivyo, pamoja na pongezi hizo bado maambukizi mapya yanaendelea na takwimu za hivi karibuni zinaonesha kwamba walau karibu wananchi 54000 wamepata maambukizi mapya. Hii taarifa nzuri. Basi nilikuwa naomba Serikali iendelee na juhudi za kudhibiti maambukizi ya VVU na UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, lakini katika ukurasa wa 40 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, watoto 58760 wapo katika dawa za ARV. Hii sio taarifa nzuri kwani inaonekana kwamba watoto hawa walipata maambukizi kutoka kwa mama zao. Kwa hiyo basi, natambua juhudi za Serikali kwa kuona Kwamba maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto yanakuwa yanazuiwa. Kikubwa ni kwamba inabidi elimu itolewe ili kusidi hawa wakina mama waweze kufika katika vituo vya clinic mapema waweze kupata huduma mapema ili kusudi wasiweze kuwaambukiza watoto wao.

Mheshimiwa Spika, Tanzania bila maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto inawezekana. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali iendelee kutoa elimu hasa katika maeneo ya pembezoni. Kwa sababu tunaamini kabia mijini wanapata elimu lakini pia maeneo ya pembezoni wanapata elimu lakini wanahitaji elimu zaidi ili kusudi waweze kupata huduma mapema na mwisho wa siku maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto yanaweza kuzuiwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, ambalo nilitaka kuzungumzia kuhusiana na hili suala la UKIMWI ni kuhusu huduma ya early infant diagnosis ambapo watoto wachanga waliozaliowa na wakinamama wenye VVU hupimwa kwa kutumia vinasaba. Taarifa imebainishwa ya kwamba vituo viko 130 na vinaendelea kutoa huduma lakini ili kuweza kufikia malengo Serikali inatamani kuwa na vituo 340 na hii itasaidia kupunguza maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto hasa maeneo ya pembezoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, Serikali basi iweze ku– speed up kuhakikisha kwamba vituo hivi vinajengwa kwa wakati ili kusudi wakinamama wale ambao wana maambukizi waweze kupimwa na hatimae wakishajua hali zao waweze kupata zile huduma ili kusudi mwisho wa siku watoto wao wasiweze kupata maambukizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niseme kwamba naunga mkono hoja ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mhifadhi namba moja, Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ana dhamira ya dhati kabisa ya kuhakikisha kwamba sekta ya utalii inaipatia pato la uhakika nchi yetu; hongera sana kwa Mheshimiwa Rais. Tumeona kabisa kwamba ile Filamu yake ya Royal Tour imesaidia kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia na hivyo kubainisha baadhi ya vivutio ambavyo viko nchini mwetu. Kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi hii nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba pia nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, watendaji wote na taasisi zote za Wizara hii kwa kuandaa hotuba nzuri ambayo imesheheni taarifa mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nizungumzie kuhusiana na suala zima la biashara ya uwindaji wa kitalii. Biashara hii ilishamiri sana miaka ya 2008 hadi 2009, kwamba Idara ya Wanyamapori iliweza kupata hadi jumla ya shilingi bilioni 60 kwa mwaka wakati biashara hii ilipokuwa ikifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa masikitiko makubwa sana, kuanzia mwaka 2013 hadi 2014, biashara hii ya uwindaji wa kitalii ilipungua na hatimaye ilikuwa ikipatikana kama bilioni 20 kwa mwaka, hapa ilisuasua kidogo. Lakini niendelee kuipongeza sana TAWA kwa kazi ambayo imekuwa ikiifanya, kwamba sasa hivi wamejitahidi tena kuweza kuoneza pato kwa biashara ya uwindaji wa kitalii kwa shilingi bilioni 60. Hii ni hatua nzuri lakini bado mimi natamani sana kwa kile kipindi cha mpito tungeweza tukafika hatua kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi bahati nzuri nilishawahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Manyoni, na kule kulikuwa kuna vitalu ambavyo vilikuwa kwa ajili ya uwindaji wa kitalii; kwa hiyo walikuwa wanakuja wageni wengi sana katika kipindi kile, na hivyo kutuletea pato la Kitaifa. Lakini pia katika yale maeneo yanayozunguka pale walikuwa wanafaidika sana wale wananchi kwa kuweza kuongeza kipato chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika yale maeneo ya kule maporini, unaweza ukashangaa kwa sababu ndege zilikuwa zinakuja, wageni walikuwa wanakuja, watu mbalimbali walikuwa wanakuja kwa ajili ya kuwinda, na hata nakumbuka ilishawahi kutokea Rais wa Panama alishawahi kuja na binti yake kwa ajili ya utalii na delegation kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi naomba niendelee kuishauri Serikali kwamba Wizara ione umuhimu wa kuiongezea bajeti TAWA ili waweze kuweka mipango yao vizuri ili waweze kujitanua zaidi katika kuweza kugawa hivi vitalu vya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa, niendelee kuipongeza TAWA kwa sababu wameweza kutumia mfumo wa kielektroniki katika kusimamia ugawaji wa vitalu vile vya utalii; hii ni hatua kubwa. Kwa hiyo natamani wapatikane wataalamu wengi zaidi waweze kusaidia ukagwaji wa vitalu hivi ili mwisho wa siku tuweze kupata faida kubwa sana. Kwa hiyo naipongeza sana TAWA kwa hatua nzuri ambayo wameifikia. Naamini kwamba kama tutakwenda hivi vizuri basi tunaweza tukapata fedha zaidi ya bilioni 120 na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu mwingine ni kwamba inabidi pia TAWA ibuni njia nyinginezo za mapato, kama vile utalii wa picha. Mfano ile Game Reserve ya Maswa ni nzuri kwa ajili ya utalii wa picha, kwa hiyo kama wataona huu ushauri unafaa basi waweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia hii Taasisi ya TAWA yale maeneo mengine waweze kufanya tathmini ya kina ili shirika liweze kuyatumia maeneo hayo kwa aina nyingine ya utalii badala ya kutegemea utalii wa uwindaji tu. Natambua kwamba kuna baadhi ya mataifa makubwa ambayo yamekuwa yakifanya kampeni hasi dhidi ya uwindaji wa kitalii, lakini hii ni miongoni mwa mbinu moja wapo katika utalii ambayo inaweza kuliletea pato kubwa sana Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninataka kulizungumzia ni vivutio vinginevyo. Kuna baadhi ya vivutio ambavyo inabidi viendelezwe. Tumeona kabisa kwamba tumejikita zaidi kwa wanyamapori na mambo mengine kidogo, lakini pia sisi tuna makabila mengi sana hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tuna makabila zaidi ya 120, tuna mila na desturi zetu; kwa nini pia tusiwekeze kwenye utalii wa makabila ili wale watalii watakapokua wanakuja waweze pia kuona makabila yetu, mila zao na desturi wanafanya nini? Tuna makabila tofauti; tuna Wamasai, tuna Wagogo, tuna Wanyamwezi, tuna Wasukuma, tuna Waha, Wamakonde, Wangoni na makabila mengi. Kama tukiweza kuonesha zile mila zao na desturi, wote hawa mimi naamini kabisa kwamba watalii hawa wataweza kwenda wakitoka kule mbugani wataweza kuona hizi mila na desturi. Labda na sisi tupeleke watu wetu, waende Ethiopia na Afrika Kusini ambako wenzetu kule wameweza kufanikiwa sana kwenye hili suala zima la mila na desturi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri utafiti ufanyike, kwamba kwa nini asilimia 20 ya watalii ambao wanatembelea katika vivutio vyetu hurudi tena kwa mara ya pili. Kwa sababu tunatamani kwamba kama wamefurahia ile hali waliyoikuta katika mbuga zetu lakini pengine kama tukaweka kwenye suala la malikale, lakini pia tukaweka labda kwenye suala la makabila, na mengineyo mengi, watalii hawa watakuwa na hamu kwamba akitoka inawezekana kabisa akakaa zile siku alizoziweka kati ya 10 au 15, kumbe ana sababu ya kwenda maeneo mengi zaidi akaongeza zile siku za kuweza kukaa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi ninashauri kwamba basi ufanyike utafiti wa kina kujua, je, ni vivutio vipi ambavyo vitaweza kuwasaidia hawa watalii waweze kurudi tena, isiwe mara moja tu, iwe mara mbili, mara tatu, mara nne, hata mara kumi? Na ikiwezekana waende wakawaambie wenzao ili waweze kufika na kuweza kufanya huo utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda si rafiki sana, mimi naomba nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa fursa, naunga mkono hoja na ninaamini kabisa kwa jinsi hali ilivyo Tanzania itaweza kufikia zaidi ya watalii milioni tano, hata milioni 10 au milioni 15 kama katika nchi nyingine zozote duniani ambazo zimeweza kufaidika na utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa fursa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu, hoja ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.

Mheshimiwa Spika, nami pia naomba niungane na wenzangu wote waliotangulia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuona umuhimu wa kuiunda upya tena Wizara hii na tumeona kabisa faida ya kuundwa Wizara hii na tunaona viongozi ambao wamekuwa wakifanya kazi katika Wizara hii jinsi wanavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa sana ambayo wanaifanya, lakini pia kuandaa bajeti hii. Mimi naomba nijikite katika masuala mawili, kwenye suala la ukatili, lakini sambamba na hilo, uanzishwaji wa madawati ya jinsia katika vyuo vya elimu ya juu na elimu ya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzagu wengi wamezungumzia, mimi pia naomba nipongeze mikakati mbalimbali ya Serikali ya kuhakikisha ukatili unatokomezwa kwa mpango mkakati yaani wa MTAKUWWA ambao dhamira ya mkakati huu ni kuhakikisha kwamba, ukatili dhidi ya wanawake na watoto unapungua kwa asilimia 50 ifikapo Juni, 2022. Nina taarifa kuwa tathmini ya mkakati huu iko kwenye stage ya consultant kwamba wako kwenye inception report, naamini kabisa ripoti hii itakapotoka itatuonesha hali halisi ya ukatili ilivyo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa nane wa taarifa hii umezungumzia kuendelea na kampeni ya kutokomeza ukatili; nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, kwa kweli hata hivyo kama walivyozungumza wenzangu kumekuwa na ukatili wa kingono, ukatili wa vipigo, kuuawa wanawake na wenza wao au waume pia, kuchomwa moto kwa watoto, lakini pia ukeketaji, usafirishaji haramu wa watoto, ubakaji na ulawiti. Ukweli ni kuwa ukatili umekithiri kupita kiasi, na pia, kwa kuwa vyombo vya habari vimekuwa vikitoa taarifa mbalimbali, matukio yamekuwa yakiripotiwa, utakuta kwamba baba, ndugu wa karibu, wanabaka na kulawiti.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, hivi karibuni kuna matukio ambayo yameripotiwa, mfano Mkoa wa Kilimanjaro kuna mume amemuua mkewe mbele yam toto wake wa miaka minne. Sasa je, huyu mtoto akikua akili yake itakuwaje?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo ni tatizo, lakini pia kuna mwanaume ambaye amemuua mke wake kwa kumpiga risasi saba, hili tukio limetokea hivi karibuni. Sambamba na hili tarehe 5 Mei, 2022 kuna mfanyakazi kuke Dar es Salaam wa baa aliuawa na mpenzi wake. Tarehe 26 Machi mtoto alinyongwa, lakini sambamba na hilo kuna baba ambaye alimvunja mtoto wake shingo kwa kushindwa kusoma, sasa sijui yeye amesoma kiasi gani mpaka akamuue mtoto wake!

Mheshimiwa Spika, lakini pia unaona kwamba, tunawapa ndugu zetu, rafiki zetu kuweza kutusaidia kutulelea watoto wetu, kuna mama mkubwa naye amemuua mtoto wa mdogo wake. Kwa hiyo, haya mambo kwa kweli, yanatisha.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, ukurasa wa nne wa hotuba hii pia umezungumzia kuhusu utekelezaji wa MTAKUWWA ambao ulianzia Julai, 2017 na utafikia ukomo mwaka 2022, lakini bado kesi zinaonekana zinaripotiwa, nyingine hazifikiwi uamuzi. Kwa hiyo, taarifa pia inaendelea kusema kwamba, pamoja na matukio kupungua kutoka 42,414 mwaka 2020 hadi kufikia 29,373 mwaka 2021, lakini pamoja na takwimu hizo tunazozipata bado ukatili upo. Kwa hiyo, matukio haya tunayapata kwa sababu ya Serikali kufanya kazi kubwa sana ya kuelimisha jamii ili kusudi iweze kutoa taarifa. Kwa hiyo, naendelea kuipongeza Serikali, lakini wito wangu ni kwamba inabidi lazima elimu iendelee kutolewa ili kusudi jamii iweze kuachana na matatizo haya ya ukatili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kulizungumzia pia, katika shule zetu. Katika baadhi ya shule nako sio salama kwenye madarasa kwa sababu, kuna baadhi ya watoto ambao madarasa ya juu wamekuwa wakiwalawiti watoto wa madarasa ya chini, na hili jambo nalo inabidi lazima tuliangalie kwa kuona jinsi gani tunaielimisha hii jamii jamani kwa sababu hawa watoto inawezekana kuna baadhi ya tabia wanazirithi kutoka katika nyumba zao au katika familia zao. Kwa hiyo, ni budi sasa ifikie wakati jamii ibadilike.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ushauri wangu ni kwamba kwanza niseme Tanzania bila ukatili inawezekana. Kila mtu akichukua nafasi yake, kila mtu kuanzia kwenye ngazi ya familia tuhakikishe kwamba tunawalea watoto wetu vizuri ili kusudi tuweze kupambana na ukaktili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ushauri wangu Sheria ya Kanuni ya Adhabu kuhusu mimba zinazotokana na kubakwa na ndugu wa damu,yaani mahirimu akiwemo baba, mjomba, kaka, baba mkubwa, iangaliwe upya ili iwaondolee sonona wale mabinti na kama itafaa ujauzito huo utolewe na wataalam.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nililokuwa napenda kupendekeza wazazi wa kiume wanaotelekeza watoto wao wawajibishwe, kwa sababu hii pia inasaidia sana kwenye suala zima la ukatili kwa sababu, baadhi ya akinamama wanashindwa kuwalea watoto wao.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine naomba nishauri, sheria iangalie jinsi ya kushughulikia madalali wanaosafirisha wasichana wa kazi, kwa sababu wasichana wa kazi nao wamekuwa wakipata madhifa sana huko wanakokwenda. Wengine wanauawa, wengine wanapewa mimba na kufanyiwa ukatili wa aina mbalibali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine, Serikali iangalie jinsi ya kutoa ulinzi na usalama kwa wanawake na watoto ambao wanatetea haki za binadamu. Kwa sababu kuna wengine huwa wanapewa vitisho ili kusudi wasiweze kwenda kutekeleza majukumu yao hasa na wale ndugu wa wahanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine ni kwamba vyombo vya kupambana na rushwa vifuatilie mienendo ya kesi za ukatili wa ngono na ubakaji, kwani kesi nyingi zinapoteza ushahidi, kwamba hawa watu ambao wanafanya hivi vitendo vya ukatili mara nyingi wengine wanakuwa na uwezo wa kipesa au ndugu zao kwa hiyo, inafikia wakati kwamba, haki inakiukwa kwa hiyo, wale ambao ni waathirika wanashindwa kupata haki yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine nilikuwa nashauri Serikali ione umuhimu wa kujenga nyumba salama za wahanga wa ukatili iwapo mtu atafanyiwa ukatili asirudi nyumbani, kwani akirudi nyumbani ndugu watakwenda pale wamrubuni, ili kusudi aweze kubadilisha mawazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watoto wapewe mafunzo ya kujilinda mapema; kwamba tuwafundishe watoto wetu katika ngazi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Naomba nimalizie. Tuwafundishe watoto wetu ili kusudi waweze kujilinda…

SPIKA: Sekunde 30; muda wako umeshaisha.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia hoja ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Nami niungane na Wabunge wenzangu kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa kuandaa bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo muda ukiniruhusu nitaongelea kuhusu Royal Tour na pia nitazungumzia kuhusu uendelezaji wa fukwe pamoja na umuhimu wa mafunzo mara kwa mara watoa huduma wa kitalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye ni mhusika mkuu katika filamu hii ya Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ana dhamira ya dhati ya kutangaza utalii wa Tanzania na vivutio vyake ili kuliongezea pato Taifa letu, pongezi sana kwa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameimarisha utalii katika Tanzania katika ile filamu ya Royal Tour sambamba na hilo Mheshimiwa Rais ameibeba Wizara ya Maliasili na Utalii katika nchi yetu pia Mheshimiwa Rais ameiweka Tanzania katika anga za kimataifa kwa kuitangaza hii filamu ya Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Rais pia amevutia wawekezaji wengi sana, ninaamini kabisa baada ya hii filamu ya Royal Tour watalii wengi wameanza kuja na wengine wengi sana watakuja. Halikadhalika hivi karibuni tumeona tija kwamba mwekezaji mkubwa sana kutoka Marekani ambaye ni Munir Walji amefika nchini kuhusu uwekezaji katika hoteli za kitalii. Hii ni hatua ya mwanzo na tunaamini kabisa watalii wengine wengi watakuja hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika mimi naamini watalii wataongezeka sambamba na hilo safari za ndege zitaongezeka, lakini sambamba na hilo uelewa wa Watanzania kuhusu utalii nao utaendelea kuongezeka na watalii wa ndani wa nchi yetu yaani Watanzania wengi zaidi watakwenda kutalii kwa hiyo hivyo pato la Taifa litazidi kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa ujumla hii ni faida kubwa sana kwa Royal Tour ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameifanya na tuendelee kumpongeza, tumtie shime na tuendelee kumuombea Mwenyezi Mungu ampe afya njema ili kusudi aweze kuliongoza Taifa letu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kuwa Wizara iendelee kuweka juhudi katika kutangaza na kuimarisha huduma zenye hadhi ya kimataifa, lakini sambamba na hilo wanafunzi wengi waendelee kuelimishwa umuhimu wa utalii ili kusudi wajenge tabia na wao watakapokua waweze kuwa watalii. Lakini sambamba na hilo ushauri mwingine waandishi wa habari waweze kupewa uwezo wa kuweza kuripoti habari zaidi zinazohusiana na masuala ya maliasili na utalii ili kusudi waweze kuitangaza vizuri nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo Watanzania nao pia waendelee kuhabarishwa kuhusiana na masuala ya utalii ili kusudi na wenyewe nao pindi wanapokutana na wageni waweze kuwaelezea kuhusiana na vivutio vya nchi yetu vilivyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba pia nizungumzie kuhusiana na uendelezaji wa fukwe ili kuboresha utalii; kuna haja ya Serikali kutafuta wawekezaji watakaojenga mahoteli ili kuweza kuboresha huu utalii wa fukwe kwani hii itasaidia kwamba wale wageni watakaokuwa wametoka kwenye mapori, wametoka kwenye misitu basi wanakwenda kwenye fukwe ili kusudi nako kule waweze kufanya utalii na kupumzika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilipenda kulizungumzia ni mafunzo ya mara kwa mara kwa watoa huduma za utalii, hili nalo ni eneo muhimu sana kwa sababu watalii wanaokuja sasa hivi Tanzania yaani wanaokuja kwa kurudia kwamba wakija mara ya kwanza wakitaka kurudia tena hawazidi asilimia 20. Kwa hiyo, ipo sababu ni kwamba hawa waongoza utalii waweze kupewa mafunzo zaidi ili kusudi wawe na mbinu bora zaidi za kuweza kuwavutia watalii watakaokuja mara kwa mara ili kusudi kuweza kuendeleza utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo najua kwamba wenzetu Chuo cha Mweka wameweza kutoa mafunzo haya walau kwa waongoza utalii 1,060. Kwa hiyo, naomba waongezwe wengine ili kusudi mwisho wa siku waweze kupata ujuzi na wakipata ujuzi ina maana kwamba wataweza kusaidia katika kutangaza utalii, askari wanyama pori, wale askari wa misitu na kadhalika kwa hiyo hawa wote waweze kupewa mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kuzungumzia nikuhusiana na cultural tourism. Bado hatujalitumia sana eneo hili wenzetu kwa mfano wenzetu Ethiopia asilimia 70 ya utalii wao wanategemea kwenye cultural tourism, sisi tuna makabila mengi sana na tunaamini kabisa na sisi tukijikita katika cultural tourism naamini kabisa tunaweza tukapata watalii wengi sana zaidi.

Kwa hiyo, ushauri wangu tutume wataalam watakaoenda kujifunza kwani sisi tuna makabila mengi sana kwamba ukienda kule kwa wahehe the way wanavyo dress unajua kabisa hawa wanaonekana, ukienda labda usukumani the way wanavyo dress wanajulikana, ukienda umasaini uhayanina maeneo mengine yote. Kwa hiyo, tukiwa na ile cultural tourism mimi naamini kabisa watalii wengi watakuja basi na hiyo itasaidia kuongeza tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda siyo rafiki baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, wa Mwaka 2016
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami nichangie katika hii Miswada miwili ambayo iko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba moja kwa moja nijielekeze kwenye Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya mwaka 2016, nianzie pale katika Kifungu cha pili (2) ambacho kinatoa tafsiri ya maneno yatakayotumika katika Sheria hii. Naomba ninukuu ukurasa wa 36 kwenye tafsiri ya maneno ya Chama cha Wakulima ambayo inasema kwamba maana yake ni Chama ambacho kimesajiliwa na mamlaka husika na kilichoanzishwa na watu wanaojihusisha na uzalishaji, usindikaji au biashara ya mazao maalum ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri wangu hapa kwamba kwa nini ibainishe kwamba mazao maalum ya kilimo, hapa tungeweza tukasema kwamba ni mazao ya kilimo, lakini huko kutakuwa kuna vikundi vidogo vidogo kile chama kiwe ni umbrella organization. Naona kwamba tujaribu kuliona hili na kwamba libadilishwe hapa kwa sababu kama tukisema kwamba ni mazao maalum ya kilimo ina maana kwamba itabidi yabainishwe, kama ni ufuta ubainishwe kwamba ni ufuta, kama ni alizeti au chochote basi tubainishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichangie katika Kifungu cha 18(4) naomba ninukuu, kimesema: “Endapo ugunduzi, uvumbuzi au ubunifu ni mali ya taasisi chini ya Kifungu cha (1), Taasisi inaweza, (a), (b), (c) kwamba kutoa tuzo kwa mtu yeyote aliyehusika na ugunduzi, uvumbuzi au ubunifu huu inaendelea mpaka (c).”
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba badala ya kusema kwamba hii taasisi inaweza litumike neno, ilazimike, kwamba iwapo ugunduzi au uvumbuzi au ubunifu ambao uko chini ya kifungu hiki, taasisi inalazimika kutoa tuzo, kwa sababu tukisema kwamba inaweza, ina maana kwamba hapa ni optional, kwa hiyo inawezekana kabisa kwamba mhusika katika taasisi hii anaweza asiitoe ile tuzo iwapo hata kama yule mtafiti anastahiki kupewa hiyo tuzo. Kwa hiyo, huo ulikuwa ni ushauri wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba nitoe pongezi zangu kwa Kifungu cha 24(1) na (2) ambapo sheria hii imebainisha kwamba lazima Mtafiti ambaye atatoka nje ashirikiane na Mtafiti wa kutoka Tanzania, ndani ya nchi. Kwa kweli nipongeze sana jambo hili na hili nadhani lingetumika kwa baadhi ya sheria zetu za nchi hii. Hata Sheria ya Uwekezaji na sheria zingine kwamba Watanzania wangekuwa wanashiriki au ni lazima washirikiane na wawekezaji, hili naomba niipongeze sana Wizara, hii itasaidia sana kuwapa weledi watafiti wetu na hivyo wajione kwamba wanakubalika na wanaaminika katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kutoa mapendekezo ni kwamba katika Kifungu cha 35 ambacho kinazungumzia masuala ya rufaa, naona kwamba pale kifungu kidogo cha (1), (2) na (3) cha Muswada huu ambacho kinapendekeza kwamba Waziri peke yake ndiye awe na mamlaka ya kumaliza ile rufaa. Nashauri ingewezekana kwamba hata Mahakama kwa sababu Waziri ni binadamu na yeye, kwa kuwa ni binadamu inawezekana kabisa kuna vitu vingine na yeye anaweza akakosea, nashauri kwamba kwenye suala la rufaa ingekwenda zaidi kwenye Mahakama nayo ipewe mamlaka ya kutoa rufaa kwa mtu ambaye atahitaji kupata rufaa hiyo badala ya kuwa Waziri peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kupendekeza kwenye Kifungu cha 36 Kifungu (1), (2) pia nikiangalia zile herufi kuanzia (a) mpaka (m) kwamba, kwa kuwa Muswada umependekeza Kifungu kitekelezwe kupitia Kanuni zitakazotungwa na Waziri, nashauri pale kuna maneno yameandikwa katika Muswada huu Kifungu 36 kwamba Waziri anaweza kutunga Kanuni kwa ajili ya utekelezaji mzuri wa masharti ya sheria hii. Naomba nishauri kwamba hapa siyo lazima Waziri aweze, hapana, nashauri iwe Waziri inabidi alazimike kutunga Kanuni hizi kwa sababu kama tukimpa option ina maana kwamba inawezekana asitunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni haya machache niliyoyaona, nikaona na mimi nitoe ushauri wangu otherwise nawapongeza sana. Naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa na mimi kuchangia hoja iliyo mbele yetu ya Muswada wa Sheria wa kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya mwaka 2018 [The Dodoma Capital City (Declaration) Bill of 2018].

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi naomba niseme kwa unyenyekevu mkubwa sana kwamba nampongeza sana Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuona umuhimu wa kuleta Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, mimi wakati Dodoma inatangazwa kuwa Makao Makuu, nilikuwa ni mtoto mdogo bado nikisoma shule ya msingi na niliweza kwenda kucheza pale kwenye lile jengo la CCM wakati ule lilikuwa linaitwa jengo la TANU. Leo kwa kweli nina faraja kubwa sana nimesimama hapa nikiwa nina umri wa zaidi ya miaka 55 tunapitisha Muswada huu. Nashukuru sana na nimefarijika sana kwamba leo ninaandika historia kwamba nilipokuwa mtoto mdogo lilitangazwa tangazo hili la kuhamia Dodoma na sasa leo mimi ni mmojawapo wa watunga sheria ambaye nasimamia Muswada huu ili uweze kupitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzangu wengi wamezungumza kwa kweli upitishwaji au uletwaji wa sheria hii ambayo tutaipisha leo hii utaleta tija kubwa sana katika Mji wetu huu wa Dodoma ambao tunaamini kabisa kwa sasa hivi ndiyo Makao Makuu ya nchi yetu. Ni ukweli usiopingika kwamba Dodoma, kama wenzangu walivyosema, ni mji ambao uko katikati lakini sambamba na hilo Dodoma ni mji ambao mpaka sasa hivi haujawa polluted hasa kwenye suala la ardhi kwani maeneo mengi sana yamepimwa, kwa hiyo, hatutegemei squatters kama ilivyokuwa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naamni kabisa sheria hii itasaidia zaidi kuendeleza na kuweka yale maeneo yote ya miundombinu ili kusudi Dodoma iwe ina sura tofauti. Naamini kabisa kwa sheria hii itasaidia kuifanya Dodoma
yetu kuwa na sura tofauti kulinganisha na Makao Makuu ya Miji mingine yote duniani. Naamini kabisa kwamba upitishwaji wa sheria hii, wawekezaji wengi sana watakuja kuwekeza hapa Dodoma, kwa hiyo, fursa nyingi zitapatikana, akina mama, vijana watafanya kazi mbalimbali. Kwa hiyo, naomba niungane na wenzangu wote kusema kwamba sheria hii itasaidia sana.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo naomba tu nitoe ushauri, kwamba sheria hii ikipitishwa Serikali itabidi ione ile mipango kabambe ya uendelezaji wa Mji Mkuu wa Dodoma isiwe tena ya miaka mitano, mitano au kumi au
25. Itabidi tuiangalie Dodoma ya miaka 100 inayokuja ili kusudi sasa ile miundombinu itakayowekwa kadri watu wataendelea kuongezeka basi ile miundombinu iwe inatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia katika kupitishwa kwa sheria hii ni kwamba, tunajua kabisa kuna ule mpango kabambe wa kuikijanisha Dodoma, yaani Dodoma iwe kijani. Kwa hiyo, kutokana na sheria hii, naamini kabisa ile mipango tuliyonayo pamoja na ule mpango wa Ofisi ya Makamu wa Rais wa kuikijanisha Dodoma tukiweka mkakati kabambe wa kuhakikisha kwamba zile Wilaya zote ambazo ziko ndani ya Makao Makuu ya Mji wa Dodoma nazo zikajitahidi kupanda miti kwa jinsi itavyoweza ili kuikijanisha Dodoma itakuwa bora zaidi. Ikiwezekana sasa ule upandaji wa miti kwa mfano wa malengo wa kupanda miti 1,500 ikapandwa lakini uwepo ufuatiliaji wa kuhakikisha kwamba ile miti 1500 yote inamea na inaendelea, hivyo tutaweza kuikijanisha Dodoma. Tukipanda miti ile tufanye ufuatiliaji na kufanya tathimini. Kwa hiyo, naendelea kuipongeza sana Serikali kwa kuweza kuleta Muswada huu hapa leo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, jambo lingine ambalo nilikuwa naomba Serikali ni kwamba, sheria hii ikipitishwa, kwa kuwa tunataka sasa Makao Makuu yaweze kuendelea kwa haraka Serikali ione namna ya kupunguza bei ya vifaa vya ujenzi ili kusudi sasa wale wawekezaji ambao wanakuja kuwekeza hapa waweze kujenga majengo mbambali. Si kwa wawekezaji tu bali hata wale wananchi ambao watakuwa na nia ya kuja kuendeleza Dodoma kwa kuweka miundombinu mbalimbali basi Serikali ione jinsi gani itakavyoweza kupunguza bei ya vifaa mbalimbali vya ujenzi ili kusudi wananchi waweze kuendeleza huu Mji wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakika naomba niendelee tena kukushukuru sana kwa kunipa fursa lakini mimi ya kwangu yalikuwa ni hayo, naendelea kuunga mkono hoja, ahsante sana.