Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Lucy Simon Magereli (2 total)

MHE. LUCY S. MAGERELI:
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la moja kwa moja kwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu , Mpango wa Serikali wa Miaka Mitano ni kuipeleka Tanzania kuwa Tanzania ya viwanda na ziko changamoto zinazokabli mpango huo na moja ni namna ya kuwawezesha wazalishaji na wafungashaji wadogo katika level za Halmashauri kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa.
Tunafahamu uwepo wa GS1 ambayo inalengo la kuwasaidia wazalishaji na wafungashaji hao kupata barcodes ili waweze kuuza bidhaa zao. Mwaka jana Waziri Mheshimiwa Mizengo Pinda alitoa maelekezo ya maandishi akielekeza TAMISEMI iagize halmashauri zote zitoe
ushirikiano kwa GS1 ili waweze kuwasaidia hao wazalishaji na wafungashaji wadogo kupata barcodes kitu ambacho kinge-stimulate uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo...
SPIKA:
Mheshimiwa Lucy sasa swali.
MHE. LUCY S. MAGERELI:
Mheshimiwa Spika ahsante, ningetemani nimalizie, anyway.
Nini sasa Kauli ya Serikali hasa kwa Ofisi ya Waziri Mkuu katika kusimamia na kutekeleza maelekezo haya ambayo tayari yalishatolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu aliyepita ili kuwasaidia wazalishaji na wafungashaji wadogo hawa?
WAZIRI MKUU:
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Ni kweli kwamba Serikali inayo mkakati, tunaendelea kuhamasisha wajasiriamali wadogo kujiendeleza kupitia viwanda vidogo vidogo na msisitizo huu wa Serikali wa viwanda unajumuisha viwanda vikubwa, vya kati na vidogo kwa lengo lile lile la kumtaka Mtanzania aweze kunufaika na hasa katika kuongeza thamani ya mazao ambayo tunayazalisha nchini.
Tumeendelea kuwa na mipango mbalimbali ambayo Serikali inaunga mkono jitihada za wazalishaji wadogo ikiwemo na uwekaji wa barcodes ambayo pia inamsaidia kupata bei na thamani nzuri ya mazao ambayo mjasiriamali anajihusisha katika kuchakata kwenye michakato ya awali kwa maana processing hii ya awali.
Mheshimiwa Spika, mkakati huu bado unaendelea na tumeagiza utaratibu huu wa
barcodes uendelee lakini pia tumehusisha TBS, TFDA kuhakikisha kwamba chakula tunachokizalisha kinakuwa na ubora ili tukikipa barcode, Taifa liweze kuuza bidhaa hiyo nje ya nchi na ndani ya nchi ambako tunaweza kupata fedha nyingi na wajasiriamali waweze kunufaika zaidi.
Kwa hiyo, nataka nikuhakikishie tu kwamba utaratibu huo bado unaendelea ili kuweza kuipa thamani mazo yetu lakini kuwapa uwezo mkubwa wa kusafirisha bidhaa zao nje na kuzipa soko ili ziweze kuwaletea tija Watanzania na tutaendelea pia kusimamia jambo hilo kuwa linaendelea kukamilika. Ahsante sana.
MHE. LUCY S. MAGERELI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Siku ya Jumatatu tarehe 4 Februari, 2019, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wakati wa majumuisho ya Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Miundombinu na Kamati ya Viwanda na Biashara alitoa kauli ndani ya Bunge lako iliyomaanisha kusema Serikali imejidhatiti kukuza mitaji yake yenyewe ili kuacha kutegemea mitaji ya uwekezaji na misaada kutoka nje na alitamka akisema wawekezaji wengi ni wezi na wana mikataba ya kinyonyaji. Je, huo ndiyo msimamo wa Serikali kuhusu wafadhili na wawekezaji wa nchi hii?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba sina uhakika kama Naibu Waziri wetu aliwahi kutoa kauli hiyo kwa sababu huo siyo msimamo wa Serikali. Msimamo wa Serikali ni kukaribisha wawekezaji kuwekeza kwenye sekta zote za kibiashara na tunatoa fursa hiyo kwa mwekezaji yeyote wa ndani mwenye uwezo na wale wa nje wanakaribishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali tumefanya kazi kubwa ya kujenga mazingira ya uwekezaji mzuri hapa nchini. Tuna ardhi ya kutosha na tumetoa maelekezo katika Halmashauri zote kutenga ardhi kwa ajili ya kufungua milango ya wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye sekta ya ardhi lakini pia tuna madini na sekta nyingi ambazo kila moja anayetaka kuwekeza anao uhuru wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jukumu letu Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatengeneza mifumo rahisi ya kumwezesha mwekezaji kuwekeza biashara yake na kufanya biashara yake katika mazingira rahisi. Pia Serikali inajitahidi kukutana na wawekezaji wakati wowote kuzungumza nao ili kusikia changamoto ambazo zinawakabili kwenye uwekezaji wao. Ndiyo sababu Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ameendelea kutoa wito wa ujenzi wa uchumi wa Tanzania kupitia viwanda na sehemu kubwa ya viwanda vinawakaribisha wawekezaji ili waweze kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nitumie nafasi hii kutoa wito kwa wawekezaji wote nchini na wale wa nje kuja Tanzania kuwekeza; sekta za uwekezaji ziko nyingi, Serikali inajenga miundombinu, tumejenga barabara nzuri za kufanya biashara zao, tunaendelea kuboresha reli, Shirika la Ndege na usafiri wa majini, malengo yetu ni kumwezesha mwekezaji na mfanyabiashara huyu kufanya biashara yake katika mazingira rahisi. Kwa hiyo, huo ndiyo msimamo wa Serikali wa kuhamasisha uwekezaji na kwamba tutawalinda wawekezaji wale wanaojenga viwanda vya ndani na tutalinda viwanda vya ndani ili viweze kufanya biashara yake vizuri zaidi. Ahsante sana. (Makofi)