Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Desderius John Mipata (16 total)

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wakati akiwa Makao Makuu ya Jimbo la Nkasi Kusini, Makamu wa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, aliwaahidi wananchi wa Jimbo hili mawasiliano ya simu za mkononi kwa Kata nne za mwambao wa Ziwa Tanganyika ambazo ni Ninde, Wampembe, Kizumbi na Kala; je, ni lini utekelezaji wa ahadi hiyo utafanyika
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata wa Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutekeleza sera ya kuzipatia huduma ya mawasiliano ya simu Kata zenye uhitaji ili kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi, wakiwemo wa Jimbo la Nkasi Kusini. Katika mwaka wa fedha wa 2015/16 Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote (UCSAF) imetenga jumla ya dola za Kimarekani 199,850 kwa ajili ya upelekaji wa mawasiliano katika Kata ya Ninde katika Awamu ya Pili A ya mradi huo. Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom Tanzania ndiyo iliyopewa zabuni ya kupeleka mawasiliano katika Kata hiyo. Mradi ulianza kutekelezwa kuanzia mwezi Aprili, 2015 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kata za Wampembe, Kizumbi na Kala, zimejumuishwa katika mradi wa mawasiliano vijijini Awamu ya Kwanza A (Phase I A) wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote na maandalizi ya ujenzi wa mnara yanaendelea chini ya kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom Tanzania. Kwa sasa Vodacom wanawaandaa wakandarasi wa kutekeleza mradi huo ambao ujenzi wake umepangwa kukamilika mwezi Juni, 2016.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuza:-
Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Rukwa ilishaomba juu ya barabara za Kitosi – Wampembe na Nkana – Kala kuchukuliwa na Mkoa na Serikali imeendelea kuzifanyia matengenezo ya dharura ili zipitike na kilio cha barabara hizo kilifikishwa kwa Rais pamoja na Makamu wa Rais wa Awamu ya Tano na wote walitoa ahadi ya kuboresha barabara hizo:-
(i) Je, Serikali ina mpango wowote wa kuzipandisha hadhi barabara hizo?
(ii) Je, ni lini Serikali itaitikia kilio hiki cha wananchi wanaopata shida kwa barabara hizo kutopitika katika kipindi chote cha mwaka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kitosi – Wampembe ina urefu wa kilometa 67 na barabara ya Nkana – Kala ina urefu wa kilometa 68 na barabara zote hizo zipo chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imepokea maombi ya kuzipandisha hadhi barabara ya Kitosi – Wampembe na Nkana – Kala kutoka Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Rukwa na baada ya kupokea maombi hayo, timu ya wataalam ilitembea barabara hizi ili kubaini iwapo zinakidhi zigezo vya kupandishwa hadhi. Maombi hayo ya kuzipandisha hadhi barabara tajwa yanafanyiwa kazi na Wizara yangu sambamba na maombi kutoka mikoa mingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imesikia kilio cha wananchi wa Wilaya ya Nkasi na inaendelea kutoa fedha za matengenezo ya barabara ya Kitosi – Wampembe. Katika mwaka wa fedha 2014/2015, Serikali ilitoa kiasi cha shilingi milioni 500 na katika mwaka wa fedha 2015/2016, shilingi milioni 300 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara hiyo kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) ili kuifanya barabara hiyo iweze kupitia katika kipindi chote cha mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015, Serikali ilitenga shilingi milioni 45 na shilingi milioni 60 zimetengwa katika mwaka wa fedha 2015/2016, kwa ajili ya matengenezo ya aina mbalimbali ya barabara ya Nkana – Kala kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ili kuhakikisha inapitika kwa kipindi chote cha mwaka.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Mamlaka ya Mji Mdogo wa Namanyere imetimiza vigezo vyote vya kuwa Halmashauri ya Mji.
Je, ni lini Serikali itaipa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Mji Mamlaka hiyo ya Mji mdogo wa Namanyere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, maombi ya kupandishwa hadhi Mamlaka ya Mji mdogo Namanyere kuwa Halmashauri ya Mji yameshapelekwa katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI baada ya kukamilika kwa vikao vya kisheria. Baada ya hatua hiyo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI itakwenda kuhakiki vigezo vinavyozingatiwa katika uanzishwaji wa Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira wakati tunakamilisha taratibu za kisheria zinazotakiwa na kufanya uhakiki kabla ya maamuzi ya kuanzisha Halmashauri ya Mji kufikiwa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wizara ya Fedha katika juhudi zake za kukusanya mapato ya Serikali, imeweka Sheria ya Kukusanya Kodi ya Magari inayoitwa Motor Vehicle au Road License. Kodi hiyo imekuwa ikilalamikiwa sana na wananchi kwa kuwa imekuwa ikidaiwa hata kwa magari mabovu au ambayo yamepaki kwa muda wote bila kujali kipindi ambacho gari lilikaa bila kufanya kazi:-
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuitazama upya sheria hii?
(b) Kwa kuwa kodi hudaiwa hata kipindi ambacho gari halifanyi kazi: Je, Serikali haioni kwa kufanya hivyo inawaibia wananchi wake?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kodi ya Motor vehicle Annual License inasimamiwa chini ya Sheria ya Road Traffic Act, 1973 pamoja na kanuni zake (The Road Traffic na Motor Vehicle Registration Regulations). Sheria hii imekuwa ikifanyiwa marekebisho mara kwa mara kulingana na mahitaji ya wakati husika. Kodi hii ni moja ya kodi zinazokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania na kutumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini na kutoa huduma mbalimbali. Hivyo hatuwaibii wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa The Road Traffic Motor Vehicle Registration Regulations ya mwaka 2001, Sura ya Pili, Kifungu cha (4) na (5) hakuna msamaha wa leseni ya gari kwa mtu yeyote na inataka ada hiyo kulipwa kila mwaka tangu gari husika liliposajiliwa. Hivyo, sheria haitoi unafuu wowote kwa gari lililosimama kwa muda mrefu bila kutembea barabarani. Ni kweli utekelezaji wa sheria hii unaleta adha kwa wamiliki wa magari na hasa pale ambapo kuna ushahidi wa kutosha kwamba gari husika limesimama kwa muda mrefu na kwa sababu za msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa adha hii, Mamlaka ya Mapato imeanza mchakato wa kuboresha sheria hii ikiwa ni pamoja na kutoa mapendekezo ya namna bora ya kuhudumia wamiliki wa magari ambayo yatakuwa yamesimama kwa kipindi kirefu bila kutembea barabarani kwa sababu za msingi. Aidha, baada ya taratibu zote kukamilika, mapendekezo ya mabadiliko ya sheria hii yataletwa Bungeni ili kujadiliwa na kuidhinishwa na Bunge lako Tukufu kwa kadri itakavyoonekana inafaa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:- Katika kampeni zake za kutafuta Urais, Mheshimiwa Rais, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli aliwaahidi wananchi wakulima na wavuvi kuboresha maisha yao, ikiwa ni pamoja na kununua mazao na kusaidia vifaa vya uvuvi kwa bei nafuu na mikopo kwa wavuvi. (a) Je, katika bajeti ya mwaka huu azima hii imezingatiwa? (b) Je, ni fedha kiasi gani itatengwa kwa ajili ya kununulia mazao? (c) Je, ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya mkopo kwa wananchi wanaojishughulisha na uvuvi hasa wale wa mwambao wa Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendeleza jitihada zake za kuwajengea mazingira mazuri wakulima na wavuvi na kuhakikisha gharama kubwa za pembejeo na vyombo vya uvuvi zinapungua ili waweze kuzipata kwa bei nafuu kwa kutenga kiasi cha milioni 100 kwa ajili ya ruzuku ya zana za uvuvi, na jumla ya shilingi bilioni 26.99 kwa ajili ya ununuzi wa mazao katika bajeti ya Wizara ya mwaka 2016/2017. Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) umetengewa shilingi bilioni 15, Bodi ya Nafaka na Mazao mchanganyiko shilingi bilioni 8.95. Aidha, ili kuongeza uwezo wa hifadhi kwa ajili ya kuwezesha kutunza mazao mengi zaidi, Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula unaendelea kukamilisha ujenzi wa ghala la Mbozi lenye uwezo wa kuhifadhi tani 5,000. Wakala pia unaongeza uwezo wa kuhifadhi kutoka tani 246,000 hadi tani 496,000 kwa kujenga vihenge na maghala katika kanda za Arusha, Shinyanga, Dodoma, Makambako, Songea na Sumbawanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haikopeshi wavuvi bali inaweka mazingira wezeshi kwa wavuvi kupata mikopo yenye riba nafuu. Aidha, Serikali kupitia Benki ya Rasilimali (TIB) imeweka Dirisha la Kilimo Kwanza kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wakulima na wavuvi. Pia Serikali imeanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo, ambayo baadhi ya majukumu yake ni kuwapatia wakulima na wavuvi mikopo yenye riba nafuu. Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepanga kutoa ruzuku kwa wavuvi kwa utaratibu wa Serikali kuchangia asilimia 40 na wavuvi kuchangia asilimia 60 ya gharama. Ruzuku hiyo itatolewa kwa kuzingatia vigezo vifuatavyo:- (i) Vikundi vya wavuvi vinavyomiliki vyombo vya uvuvi vilivyosajiliwa kisheria ambavyo vinalenga kuvua kwenye maji ya kina kirefu; (ii) Vikundi kuthibitisha uwezo wa kulipa asilimia 60 ya gharama ya vyombo na zana zilizoombwa; na (iii) Maombi husika yanatakiwa yapitishwe na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri husika. Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuhimiza vikundi vya uvuvi vilivyo katika majimbo yao vilivyokidhi vigezo kukamilisha taratibu za kuchukua engine hizo. Aidha, vikundi vingine vinashauriwa kutuma maombi kupitia Halmashauri zao na kuwasilisha Wizarani ili viweze kupata engine za uvuvi.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Hapa nchini pamekuwepo na ongezeko kubwa la Taasisi mbalimbali zinazotoa huduma za kifedha kama vile Benki, Vikundi mbalimbali kama VICOBA, Taasisi za Kukopesha Watumishi, Taasisi za kukopesha wafanyabiashara na wakati mwingine watu na mitaji yao wanakopesha watumishi (kienyeji) kwa kificho ficho:-
(a) Je, ni chombo kipi hasa chenye wajibu wa kufuatia kodi zinazotozwa na wananchi?
(b) Je, kodi zinazotozwa ni halali?
(c) Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha wananchi
wake hawaibiwi kwa njia hiyo?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la
Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini,
kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, Toleo la 2005, Ibara ya 138(1) inaelekeza kuwa, hakuna kodi ya aina yoyote itakayotozwa isipokuwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge au kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa Kisheria na uliotiwa nguvu Kisheria na Sheria iliyotungwa na Bunge
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, Sura ya 399(5) imeipatia Mamlaka ya mapato wajibu wa kukadiria, kutoza na kutoa hesabu za mapato yote ya umma. Aidha, Sheria ya bajeti kifungu cha 58(b) inaelekeza kuwa mtu yeyote aliyepewa Mamlaka ya kukusanya mapato ya Serikali atawajibika kukusanya kwa ufanisi, kutoa hesabu za mapato, kuyawasilisha na kuyatolea taarifa kwa kuzingatia Sheria husika na kuchukua tahadhari kuzuia usimamizi mbovu wa mapato na pale inapolazimu, mfano; katika operesheni maalum dhidi ya wakwepa kodi sugu au mazingira hatarishi, TRA inaweza kuomba msaada wa vyombo vingine vya dola.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kodi halali zinazotozwa kwenye huduma za kifedha kwa mujibu wa Sheria ni zifuatazo:- Kodi ya zuio kwenye faida inayolipwa kwa Mwekezaji ambayo ni pamoja na amana za Benki, dhamana za Makampuni au Serikali na hisa; Kodi za ongezeko la thamani kwenye ada zinazotozwa kwenye huduma za kifedha na ushuru wa bidhaa kwenye ada inayotolewa kwenye kutuma au kupokea fedha kwa njia za kielektroniki na hususani simu za mkononi.
Mheshimiwa Naibu Spika, endapo mtu binafsi ama
Taasisi itatoza ama kukusanya kodi yoyote kinyume na matakwa ya Sheria, anakuwa ametenda kosa na hatua stahiki zinapaswa kuchukuliwa mara moja dhidi yake.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Nne iliahidi kupeleka maji katika vijiji vya Nkata, Ntemba, Kitosi, Ntuchi, Isale hadi Msilihofu kupitia mradi uliokuwa na thamani ya shilingi bilioni 2.8 na vilevile ahadi hiyo imetolewa na Serikali ya Awamu ya Tano.
Je, mradi huo umefikia hatua gani?
Je, ni lini hasa wananchi wategemee kutatuliwa kwa kero yao ya ukosefu wa maji safi kupitia mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mradi wa maji wa Isale ulisanifiwa mwaka 2013 katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kupitia mpango wa vijiji kumi kwa kila Halmashauri. Mradi huu ulilenga kukipatia maji Kijiji cha Isale kutoka Mto Nzuma. Mwaka 2014 utekelezaji wa mradi huu ulisimama kwa muda ili kufanya mapitio ya usanifu wa mradi utakaojumuisha pia mahitaji ya huduma ya maji kwa wananchi wa vijiji vya Ntuchi, Nkata, Mtemba na Msilihofu.
Mheshimiwa Spika, taarifa ya awali ya usanifu iliwaislishwa na Mtaalam Mshauri na kujadiliwa kwa pamoja na Halmashauri na Mkoa ambapo Mtaalam Mshauri ameelekezwa kufanya marekebisho ili kukidhi mahitaji halisi ya vijiji vyote. Mapitio ya usanifu yatakamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2017 na mradi utatekelezwa katika Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji iliyoanza kutekelezwa mwezi Julai, 2016 na utakapokamilika utatatua kero ya ukosefu wa maji safi kwa wananchi wa Nkasi Kusini.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Suala la ufugaji samaki lina faida nyingi kwa wananchi kama kujiongezea kipato na kupata kitoweo lakini wananchi wa Kata za Ninde, Kala, Wampembe na Kizumbi walioko kando ya Ziwa Tanganyika hawafugi samaki kwa kukosa elimu:-
Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam kutoa elimu ya ufugaji samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa shughuli za ufugaji wa samaki zina faida nyingi kwa wananchi zikiwemo kujipatia ajira, lishe na kipato. Wilaya ya Nkasi ni moja ya Wilaya zenye mazingira na maeneo mazuri kwa ajili ya ufugaji wa samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ina wataalam wa uvuvi saba, wawili kati ya hao wana shahada ya ukuzaji wa viumbe kwenye maji na watano wana diploma zinazohusiana na masuala ya uvuvi na ufugaji wa samaki. Aidha, Kituo cha Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (doria) cha Kipili kilichopo katika Wilaya ya Nkasi chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kina wataalam watano. Pamoja na shughuli za usimamizi wa rasilimali za uvuvi katika Ziwa Tanganyika, watumishi hao wana jukumu la kusimamia shughuli za ufugaji wa samaki ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za ugani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza kasi ya utoaji elimu ya ufugaji wa samaki katika ukanda wa mwambao mwa Ziwa Tanganyika, Serikali kupitia Wakala wa Elimu ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) ilianzisha kituo cha FETA Kibirizi – Kigoma ambapo mwaka 2015/2016 kilidahili wanafunzi 59 na wanafunzi 29 walihitimu masomo yao na katika mwaka 2016/2017 walidahili wanafunzi 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Kituo cha Ukuzaji Viumbe kwenye Maji kilichopo Manispaa ya Kigoma kwa kushirikiana na Halmashauri zilizoko kwenye ukanda huo kimehamasisha ufugaji wa samaki na kuzalisha vifaranga vya samaki 31,404, ambapo katika mwaka 2016/2017, Wilaya ya Nkasi jumla ya wananchi 70 walipata elimu ya ufugaji wa samaki katika Vijiji vitatu vya Ninde, Msamba, Namansi ambao wameanzisha kikundi kimoja katika Kitongoji cha Chele. Katika Kata ya Kala jumla ya watu 270 kutoka Vijiji sita vya Kala, Tundu, Kilambo, King’ombe na Mlambo wamepata elimu ya ufugaji wa samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na viongozi wenzake katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi katika kuweka vipaumbele na uhamasishaji wa ufugaji wa samaki ili wataalam waliopo waendelee kuhamasisha ufugaji wa samaki katika maeneo yaliyoainishwa na watumishi kutoka Wizarani tutahakikisha kwamba tunakwenda Nkasi kushirikiana nao katika kutoa huduma za ugani katika masuala ya ufugaji wa samaki. Aidha, vijana washauriwe kujiunga na mafunzo ya ufugaji wa samaki katika Kituo cha Wakala wa Elimu Mafunzo ya Ufundi (FETA) kilichopo Kibirizi – Kigoma na hatimaye waweze kujiajiri katika shughuli za ufugaji wa samaki kwa lengo la kujipatia ajira, lishe na kipato.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wananchi wa Kata ya Nkandasi wamejitahidi kujenga shule ya Sekondari ya Kata ya Milundikwa hadi kufikia kidato cha sita lakini Serikali kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeamuru shule hiyo kuhamishwa mara moja kuanzia tarehe 1 Januari, 2017 kuachia Jeshi:-
(a) Wananchi walitumia muda na rasilimali zao kukamilisha ujenzi huo na sasa wanakwenda kuanza upya: je, ni upi mchango wa Wizara kwa ujenzi mpya wa shule?
(b) Wizara ya Elimu imeafiki kuhamishwa shule hiyo ya Kata; Je, ni upi mchango wa Wizara katika uhamishaji wa shule hiyo?
(c) Je, Serikali iko tayari kufanya uthamini wa miundombinu yote ya shule na majengo, yaliyojengwa na wananchi na thamani hiyo kuitoa katika fedha taslimu kwa ujenzo wa shule mpya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deusderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Jeshi la Kujenga Taifa kuhitaji eneo lao ilipokuwa imejengwa shule ya sekondari ya Milundikwa kuanzia Januari 2017, Serikali ilihamishia shule hiyo kwenye eneo jipya la Kijiji cha Kasu A. Ushirikiano mzuri baina ya Serikali Kuu, Halmashauri, JKT, Mbunge na wananchi umewezesha ujenzi wa madarasa 13, vyoo matundu 26 na bweni moja kukamilika. Ujenzi wa maabara moja ya sayansi na bweni la pili uko katika hatua za mwisho ambapo wanafunzi 461 wakiwepo 92 wa kidato cha tano wanasoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kuchangia shilingi milioni mbili na wananchi wa Kata ya Nkandasi hususan Vijiji vya Katani, Kisula, Malongwe, Milundikwa, Kasu A na Kasu B kwa kujitolea kuchimba msingi, kukusanya mawe na mchanga, kuteka maji kwa ajili ya ujenzi kwa utaratibu wa 50 kwa 50 yaani wanaume 50, wanawake 50 kila siku ya ujenzi na kufyatua tofali za kuchoma laki mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi nayo ilitoa milioni arobaini na tisa kwa ajili ya ujenzi huo na Serikali Kuu kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ilitoa shilingi milioni mia mbili hamsini na tisa zilizotumika kujenga vyumba vya madarasa manne, vyoo matundu 22 na mabweni mawili ambapo ujenzi wa bweni la pili unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia ukamilishaji wa bweni la pili, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa mwezi Desemba, 2017 imepeleka shilingi milioni mia moja na Jeshi la Kujenga Taifa nalo lilichangia mabati 204, miche 300 ya miti kwa ajili ya mazingira na pia imetoa Walimu 10 wanajeshi ambao wanafundisha shuleni hapo. Katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, Serikali imependekeza shule hiyo itengewe shilingi milioni 230 ili kujenga maabara za sayansi mbili, jengo la utawala, bwalo na nyumba za Walimu endapo Bunge litaridhia.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wananchi wa Kata ya Nkandasi wamejitahidi kujenga Shule ya Sekondari ya Kata ya Milundikwa hadi kufikia Kidato cha Sita, lakini Serikali kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeamua shule hiyo kuhamishwa mara moja kuanzia tarehe 1 Januari, 2017 ili kuliachia Jeshi:-
(a) Je, Serikali inatoa mchango gani katika uhamishaji na ujenzi mpya wa shule hiyo?
(b) Je, Serikali iko tayari kufanya tathmini ya miundombinu yote ya shule na majengo yaliyojengwa na wananchi na thamani hiyo kuitoa katika fedha taslimu kwa ujenzi mpya wa shule?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbuge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Milundikwa lilikuwa ni Kambi ya JKT iliyokuwa ikiendesha shughuli za malezi ya vijana na uzalishaji mali kabla ya Serikali kusitisha mpango wa kuchukua vijana mwaka 1994. Wakati JKT linasitisha shughuli zake katika Kambi hiyo liliacha majengo ya ofisi na nyumba za makazi, baadaye Halmashauri ya Wilaya ilianzisha shule ya Sekondari ya Milundikwa na kuongeza miundombinu michache katika shule hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua ya kuliongezea Jeshi la Kujenga Taifa uwezo wa kuchukua vijana wengi zaidi mwezi Novemba mwaka 2016 Serikali ilitoa maelekezo kwa JKT kufufua makambi yaliyokuwa yameachwa mwaka 1994 likiwemo la Milundikwa. Kufuatia maagizo hayo ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Nkasi na Halmashauri ya Wilaya hiyo waliratibu na kusimamia utaratibu wa kuhamisha Walimu na wanafunzi waliyokuwa katika shule Milundikwa kwenda katika shule jirani. Baadhi ya wanafunzi walihamishiwa katika shule ya Sekondari ya Kasu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia maendeleo ya wanafunzi waliokuwa wakisoma katika Shule ya Sekondari ya Milundikwa mnamo tarehe 9 Februari, 2017 Wizara ya Ulinzi na JKT kupitia Makao Makuu ya JKT ilitoa mabati idadi 2,014 ili kuhakikisha kuwa vyumba vya madarasa vilivyokuwa vinaendelea kujengwa vinakamilika na kuanza kutumika. Wizara yangu itakuwa tayari kuendelea kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya katika kutoa vifaa vya ujenzi kadri uwezo utakavyoruhusu.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Serikali imetumia zaidi ya shilingi milioni 350 kuimarisha barabara ya Namanyere – Ninde yenye urefu wa kilomita 67, lakini fedha hazikutosha kukamilisha barabara hiyo:-
Je, Serikali itatenga fedha zaidi kukamilisha barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Barabara ya Namanyere- Ninde yenye urefu wa kilomita 67, kwa mara ya kwanza iliibuliwa na mradi wa TASAF Awamu ya I mwaka 2005/2006 kwa kulima barabara hiyo kwa kutumia nguvu kazi ya wananchi. Kwa kipindi chote hadi mwaka 2014/2015, barabara haikufunguka kwa kukosa miundombinu muhimu kama vile madaraja na makalvati.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, Serikali ilitenga fedha jumla ya shilingi milioni 375.3 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ambapo fedha hizo zilitumika kwa kufyeka barabara na kuondoa miti katika barabara yote, kuilima barabara kwa urefu wa kilomita 25 kwa kiwango cha udongo, kujenga Makalvati 15 pamoja na kujenga madaraja manne. Kati ya madaraja manne yaliyojengwa, mawili yapo katika Mito ya Lwafi na Ninde, hivyo matengenezo hayo yamewezesha barabara hiyo kufunguka kwa urefu wa kilomita 25 tu.
Mheshimiwa Spika, kulingana na upatikanaji wa fedha, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufanyia matengenezo barabara hiyo ambapo mwaka wa fedha 2015/2016, shilingi milioni 44.58 zilitengwa kwa ajili ya kufanya matengenezo ya muda maalum kwa urefu wa kilomita 20. Aidha, mwaka wa fedha 2016/2017, kiasi cha shilingi milioni 20 zilitumika kuimarisha sehemu korofi zenye urefu wa mita 500.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuifungua barabara hii kadri fedha zitakavyokuwa zinapatikana ili kusaidia wananchi wanaotumia barabara hii katika suala zima la usafiri.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Serikali kupitia Mradi wa Mfuko wa Benjamin Mkapa ilidhamiria kujenga na kukamilisha huduma ya upasuaji kwenye Kituo cha Afya cha Kata ya Kala na baada ya mfuko huo kuacha shughuli zake hakuna juhudi inayoendelea.
(a) Je, kuna mpango wowote kuendeleza nia hiyo njema?
(b) Kwa kuwa kituo hicho kina upungufu mkubwa wa wataalam; je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi wakiwepo wauguzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa za Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ina vituo vya afya saba, kati ya hivyo vituo vinne vinamilikiwa na taasisi za kidini na vitu vitatu vinamilikiwa na Serikali. Vituo vya afya viwili vinavyomilikiwa na Serikali vinatoa huduma za upasuaji. Kituo cha Afya Kala kinamilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Sumbawanga. Taasisi ya Benjamin Mkapa ilijenga chumba cha upasuaji (theatre) pamoja na kutoa baadhi ya vifaa kwa ajili ya huduma za upasuaji katika Kituo cha Afya Kala mnamo mwaka 2016/2017.
Hata hivyo, huduma hizo zimekuwa hazitolewi kutokana na changamoto mbalimbali kubwa zikiwa ni upatikanaji wa wataalam kwa ajili ya kufanya huduma za upasuaji na kukosekana kwa huduma ya umeme na mfumo wa maji kwa ajili ya kuendeshea shughuli za upasuaji. Ili kukabiliana na hali hiyo Halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni 17.3 katika mwaka wa fedha 2017/2018, kwa ajili ya miundombinu ya maji na umeme ambapo fedha hiyo bado haijapokelewa.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na upungufu wa watumishi katika Kituo cha Afya Kala, Halmashauri ilipeleka tabibu mmoja na wauguzi wawili ili kutoa huduma katika kituo hicho mwaka 2015. Aidha, Halmashauri ilipeleka gari moja la wagonjwa lenye namba za usajili SM 4467 mwaka 2017 kutoa huduma katika kituo hicho. Serikali itaendelea kupeleka wataalam wa afya katika kituo hicho kwa kadri watakavyopatikana. Serikali inaendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa Kituo cha Afya Kala ili kushirikiana katika kutatua changamoto ya watumishi katika kituo hicho kwa kuwa watumishi watatu waliopo sasa katika kituo hicho wote wameajiriwa na Serikali.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Hivi karibuni Mheshimiwa Rais alitoa agizo la kutatua migogoro ya vijiji na hifadhi mbalimbali na orodha ya vijiji vyenye migogoro toka Jimbo la Nkasi imefikishwa na kupokelewa na Wizara:-

Je, ni lini migogoro ya vijiji vya Kasapa, King’ombe, Mlambo, China, Nkomanchindo na vinginevyo vilivyoondoshwa vitapatiwa ufumbuzi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Mbunge anavyofahamu, utatuzi wa migogoro iliyopo katika vijiji vyote nchini na hifadhi vikiwemo vijiji Kisapa, King’ombe, Mlambo, China na Nkomanchindo umetolewa maelekezo na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kwamba mara utekelezaji wa maelekezo hayo utakapokamilika, ufumbuzi wa migogoro hiyo utakuwa umepatikana. Nitoe rai kwa wananchi kuacha kuvamia maeneo mapya ya hifadhi wakati huu, wakati migogoro huo unasubiri yanatafutiwa ufumbuzi.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Tarafa ya Wampembe ina Kata za Kala, Wampe mbe, Kizumbi na Ninde na ambazo zote ziko umbali wa zaidi ya km 80-150 kutoka Makao Makuu au mahali ambapo huduma za Mahakama zinaweza kupatikana:-

Je, ni lini Serikali itajenga walau Mahakama ya Mwanzo katika moja ya Kata hizo hususani Kata ya Wampembe ili kusogeza huduma hiyo kwa Wananchi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kuwa na huduma za haki zinazozingatia karibu na wananchi Mahakama ya Tanzania imeazimia kuwa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Mahakimu Mkazi kwa kila Mkoa, Mahakama ya Wilaya kwa Wilaya na katika ngazi za tarafa kuwa na walau Mahakama moja ya mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa ya Wampembe aliyouliza Mheshimiwa Mbunge tayari Mahakama ya Mwanzo ipo na inatumia jengo la Ofisi ya Tarafa. Ni kweli kwa muda mrefu wananchi wa Tarafa hii wamekuwa wamekuwa wakifuata huduma za Mahakama umbali mrefu. Lakini kuanzia tarehe 23 Aprili, 2018 Mahakama ya Mwanzo ya Wampembe ilifunguliwa na mpaka sasa inaendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa eneo hilo na maeneo ya jirani. Pamoja na jitihada hizo Mahakama inaendelea na kuratibu na kupata eneo katika Tarafa hiyo ili uweze kujenga jengo la Mahakama ya Mwanzo Wampembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha Wizara yangu, kwa kushirikiana na Mahakama tumepanga kujenga jengo la Mahakama ya Wilaya ya Nkasi, ambalo pia litatumika na Mahakama ya Mwanzo ya Yanamanyere. Ujenzi huu unatarajiwa kuanza mwezi Mei mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kutoa shukurani za dhati kwa Mheshimiwa Mbunge wa Halmashauri ya Wilaya kwa kujitahidi na kuuliza swali hilo na jitihada zote zinazofanyika kuwezesha upatikanaji wa jengo la kuendesha Mahakama ya Mwanzo Wampembe ambalo linatuwezesha kutoa huduma kwa wananchi wa eneo hilo na maeneo jirani wakati tukiendelea na taratibu za kupata jengo la Mahakama ahsante.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Wananchi wa Kijiji cha Kasapa walikuwa na ombi la kuongezewa maeneo ya kilimo kutoka kwenye eneo la Hifadhi ya Kalambo TFS:-

Je, Serikali imefikia hatua gani katika utekelezaji wa ombi hilo la wananchi wa Kijiji cha Kasapa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Msitu wa Kalambo River ulihifadhiwa rasmi kwa kupitia tangazo la Serikali Na. 105 la mwaka 1957. Msitu huo upo katika Wilaya ya Kalambo na Nkasi Mkoani Rukwa na una jumla ya hekta 41,958.

Mheshimiwa Spika, hifadhi hii imekuwa na umuhimu wa kipekee kwa uhifadhi wa viumbe haia na vyenye umuhimu wa kipekee wakiwemo tembo. Aidha, hifadhi ina umuhimu mkubwa katika kutoa huduma za Kiikolojia kama maji. Maji haya ni muhimu kwa matumizi ya wananchi wa eneo hilo, pia kwa ajili ya maporomoko ya Kalambo ambayo ni pili kwa urefu mita 240 Barani Afrika baada ya yale ya Victoria yaliyoko Zimbabwe.

Mheshimiwa Spika, aidha, maporomiko ya Kalambo yana upekee kwa kuwa ni moja ya vivutio muhimu ambavyo vinaendelezwa kuchangia ukuaji wa uchumi kupitia Sekta katika Mikoa ya Rukwa na Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 5 Julai, 2017 Waziri wa Maliasili na Utalii alitembelea Hifadhi ya Kalambo na baadaye Vijiji vya Kisapa ili kusikiliza maombi yao ya uhitaji wa ardhi. Katika Mkutano huo, Mheshimiwa Waziri aliagiza TFS kushirikiana na Halmashauri kufanya upimaji na tathmini ya maeneo yanayolimwa na kutoa taarifa ya mapendekezo ya hatua stahiki zitakazochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, kufuatia maelekezo hayo, TFS kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ilifanya soroveya na kubaini kuwa maeneo mengi ya vijiji hivyo yamo ndani ya hifadhi ya misitu. Katika kushughulikia changamoto ya migogoro hiyo Mheshimiwa Rais aliunda Kamati ya Wizara nane kisekta kushughulikia migogoro baina ya wananchi na hifadhi. Mojawapo ya maeneo yanayofanyiwa kazi na Kamati hiyo ni pamoja na ombi la kuongezewa ardhi kwa wananchi wa Vijiji vya Kisapa na King’ombe. Taarifa ya Kamati imewasilishwa kwa Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kupata maelekezo. Namwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira wakati tunasubiri maelekezo ya Serikali.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Vijiji vya Sintali, Nkana, Nkomachindo na Katani viko kwenye mpango wa kupata umeme wa REA Awamu ya III lakini mpaka sasa hakuna kazi zinazoendelea:-

Je, ni lini kazi hiyo itaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata Mbunge wa Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya vijiji 51 vitapatiwa umeme katika Wilaya ya Nkasi ikiwa ni pamoja na vijiji 12 vya Jimbo la Nkasi Kusini vya Ntuchi, Tambaruka, Chima, Chatelekesha, Isasa, Kingombe, Ntemba, Nkomolo II, Kasapa, Kisula, Namansi na Kasu B. hadi kufikia mwezi Mei, 2019 umeme tayari umeshawasha katika vijiji vya Chala, Chima, Chala Isasa na Ntemba. Jumla ya wateja wa awali 77 wameunganishiwa umeme. Aidha, mkandarasi anaendelea na kazi katika vijiji 9 viliovyosalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi katika Jimbo la Nkasi Kusini vinahusisha ujenzi wa kilometa 29.65 za njia ya umeme wa msongo kilovoti 33; kilometa 28 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4; ufungaji wa transfoma 14 na uunganishwaji wa wateja wa awali 324. Gharama za kazi hiyo inakadiriwa kufikia shilingi bilioni 2.15.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Sintali, Nkana, Katani na Nkomachind vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili unatarijiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.