Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Josephat Sinkamba Kandege (324 total)


MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kulichukulia kwa uzito suala hili na kutenga fedha hiyo. Imani yangu ni kwamba kifaa hiki kitakamilika na kitafika kwa wakati kwenye Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana. Sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana inao ujenzi wa jengo kubwa lenye ghorofa mbili kwa ajili ya wodi ya wanaume. Nataka commitment ya Serikali, je, watakuwa tayari baada tu ya jengo hili kukamilika mapema mwakani mwezi wa tatu kutusaidia kwa ajili ya kupata vitanda na vifaa tiba vingine ili kutoa huduma iliyo bora kuendana na kasi ya Awamu ya Tano?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Wilaya ya Ilemela haina Hospitali ya Wilaya ya Ilemela lakini ni wilaya mpya na ujenzi wa hospitali yake umeanza kwa kusuasua sana. kwenye bajeti ya shilingi bilioni nne sasa hivi imeshapata milioni 500 peke yake. Nataka kujua je, Serikali itakuwa tayari kuhakikisha fedha zipatikane na kwenda kukamilisha ujenzi wa hospitali hii ya Wilaya kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Jimbo la Ilemela?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na upatikanaji wa vifaa ni dhahiri kwamba Serikali ina nia ya dhatikuhakikisha kwamba vifaa vinapatikana ili hospitali hiyo iweze kufanya kazi iliyotarajiwa na hivi sasa ninavyoongea tayari vitanda 25 vimeshapelekwa Nyamagana pamoja na magodoro yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za Wilaya zinafanya kazi kwa kiwango cha hali ya juu kabisa. Tutakuwa tayari mara hospitali hii itakavyokuwa imekamilika tuhakikishe vifaa vyote vinapelekwa ili iweze kufanya kazi kwa ajili ya kusaidia Watanzania wa Nyamagana.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto nyingi sana za Mikoa mipya na Wilaya mpya ambazo nyingi hazina Hospitali za Wilaya. Nini kauli ya Serikali ikiwemo wilaya ya kwangu ya Tanganyika ambayo haina Hospitali ya Wilaya. Serikali ina mpango gani wa kumaliza tatizo la ukosefu wa Hospitali za Wilaya katika maeneo yote nchini ambayo hayana Hospitali za Wilaya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba afya kwa wananchi wa Tanzania kama ilivyo kipaumbele na ndiyo maana bajeti imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mpaka shilingi bilioni 269. Hii inaonesha jinsi ambavyo Serikali itahakikisha kwamba huduma hii inawafikia wananchi na kwa kuwepo Hospitali za Wilaya maeneo yote ambayo Hospitali za Wilaya hazipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizitake halmashauri zote zianze kwa kutenga maeneo lakini pia kwa kutumia own source na wao waanza ili Serikali iweze kuunga mkono jitihada hizo. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kw amajibu mazuri. Pamoja na majibu mazuri hayo napenda kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji huu bado kuna maeneo mbalimbali katika Halmashauri mbalimbali katika Mkoa wangu wa Ruvuma na maeneo mengine kwenye Halmashauri nyingine maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mpango gani wa kuwachukulia hatua kali halmashauri ambazo bado wanawanyonya kwa kuwatoza ushuru wajasiriamali wadogo wadogo wote katika Halmashauri zote zilizoko mkoani Ruvuma na maeneo mengine? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wafanyabiashara hao wadogo wadogo wanafanya biashara katika mazingira magumu sana jua la kwao, mvua ya kwao, vumbi lao. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawekea mazingira bora ili wamachinga hao waweze kuepuka adha hiyo wanayoipata? (Makofi
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi sote ni mashuhuda kwamba, Sheria hii ilipitishwa na Bunge lako Tukufu na kwa vyovyote vile hakuna kisingizio chochote ambacho kinaweza kikatolewa na halmashauri eti kwa sababu, wakidhani kwamba, sheria ndogo ambazo wao hawajazipitisha zinakuwa zinakinzana kwamba hazitawaletea mapato. Naomba niwasihi Wakurugenzi wote Halmashauri zote, na jambo hili hata Mheshimiwa Rais amekuwa akilirudia, naomba niliseme kwa mara ya mwisho; Mkurugenzi yeyote wa halmashauri iwayo yoyote ambaye atapingana na maelekezo haya na sheria aambayo imetungwa na Bunge lako Tukufu, sisi kama Serikali hatutasita kumchukulia hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili anaulizia namna ya kuwawekea mazingira mazuri wafanyabiashara wadogo wadogo. Ni dhamira ya Serikali na ndio maana tunaanza kwa kuwatambua kwa kuwapa vitambulisho ili tuhakikishe kwamba, wanatengewa maeneo mazuri ili wafanye kazi katika mazingira yaliyo mazuri kwa ajili ya kuongeza kipato cha nchi.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Pamoja na majibu yanayoridhisha ya Mheshimiwa Naibu Waziri, mimi nilikuwa tu nataka niweke msisitizo kwenye hili jambo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba, Mheshimiwa Rais amekuwa akirudia na wewe leo hapo umejaribu kuweka msisitizo, lakini bado kuna shida kule chini kwa Wakurugenzi wa Halmashauri kukataa hili agizo kwa maana circular bado haijafika.
Sasa nataka nijue tu kabisa kwamba, je, circular hiyo inahusu ile mizigo ya wakulima ama wananchi wa kawaida wenye chini ya tani moja, kama Rais alivyoagiza kwamba ukisafirisha mzigo kutoka eneo moja kwenda lingine, chini ya tani moja hutakiwi kulipa ushuru; kwa hiyo, nilitaka nijue kama circular na yenyewe inazungumzia hivyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetangulia katika jibu langu la msingi kwamba tozo hizi ziliondolewa ndani ya Bunge lako Tukufu na ndani ya Bunge hili tulisema ni tozo zipi ambazo zinafutwa kwa sababu ni kodi kero. Hakuna by-law yoyote kwenye halmashauri ambayo inazidi Sheria ambayo inatungwa na Bunge lako Tukufu. Kwa hiyo, nazidi kuomba na nawasihi wakurugenzi wote hawana option nyingine zaidi ya kutekeleza Sheria ambayo imepitishwa na Bunge lako Tukufu.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Bunge lililopita tulitunga sheria ya kufuta hotel levy, lakini katika Mkoa wa Dar-es-Salaam hotel levy imeendelea kutozwa. Na Mheshimiwa Waziri anakiri na kusema kwamba, Sheria za Bunge zinazotungwa ziheshimiwe. Nini kauli ya Waziri?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, ile Sheria ya Hotel Levy inajieleza, ukiisoma vizuri kuna definition ya hoteli, inatakiwa iwe na sifa ipi ili ikidhi kuwa hoteli. Sasa kumekuwa na mchanganyiko kati ya hoteli na guest house. Ukiisoma Sheria ya Hotel Levy inaelekeza wale ambao ni VAT registered hawatakiwi kutoa hotel levy, lakini wale ambao wako chini ya Halmashauri bado sheria imesimama. Kwa hiyo, ni suala tu la kusoma sheria vizuri na kuitafsiri vile inavyotakiwa.

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa napenda tu kutoa msisitizo kuhusiana na masuala yale ya kutoza ushuru. Nilikuwa naomba Halmashauri kwa kuwa, zenyewe ndio zinazoweka maeneo ya vizuizi na kukagua juu ya masuala ya kutoza ushuru ni vema sasa kuwe na mizani ambayo itawezesha hawa wananchi kuona kwamba mzigo wao una hiyo tani moja iliyoruhusiwa au la. Kinyume na hapo kwa kuangalia tu magunia kwa upande mmoja inakuwa inawafanya aidha wananchi wananyanyasika au wenyewe Halmashauri kutokupata ushuru ulio sahihi.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini naomba kwa sababu ndiyo nazungumza mara ya kwanza baada ya sakata la makinikia kuwa limepata mwelekeo, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa hatua alizochukua. Hatua ambazo zimekuwa ni kilio changu na kilio cha wananchi wa Msalala kwa miaka yote toka Mgodi wa Bulyanhulu ulipokuwepo pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa sababu, wananchi kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, wameitikia vizuri sana katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa huduma za afya katika Halmashauri na jimbo lao na kwa sababu, changamoto ambayo ipo ni upatikanaji wa fedha Serikalini na kwa bahati nzuri tayari tumeshapata uhakika kwamba, tutalipwa zaidi ya bilioni 700 kutika kwenye makinikia.
Je, Serikali inaweza sasa ikakubaliana na ombi langu kwamba ni vizuri tukapata angalao shilingi bilioni 3.4 ambazo zinatakiwa kuyakamilisha maboma yote haya, ili wananchi hawa wasione nguvu zao zikiharibika kwa sababu mengine yana zaidi ya miaka saba toka yalipoanzishwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa tayari tumeshaletewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya uboreshaji wa Kituo cha Afya cha Chela, fedha ambazo pamoja na kwamba ni nyingi, lakini bado hazitoshi kwa sababu, malengo ni makubwa zaidi. Je, Serikali inaweza ikakubaliana na ushauri wangu kwamba, kwa sababu lengo nikupeleka huduma kwa wananchi wengi zaidi na kuna maboma tayari kwenye Vituo vya Afya vya Isaka, Mega na Lunguya ambavyo kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri kwamba viko kwenye hatua mbalimbali. Je, Waziri anaweza akatukubalia ombi letu kwamba fedha hizi tuzigawanye kwenye hivi vituo, ili angalao navyo viweze kufunguliwa halafu uboreshaji utakuwa unaendelea awamu kwa awamu kadri fedha zinavyopatikana kuliko kukaa na kituo kimoja na vingine vikaishia kwenye maboma kama ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya ombi la uwezekano wa kutizama hii bilioni 3.4 zitumike ili kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya pamoja na zahanati; kimsingi hitaji ni kubwa sana, lakini si rahisi kabla ya kufanya hesabu kujua katika mahitaji mengine kiasi gani kiende upande wa afya, kwani vipaumbele ni vingi. Kwa hiyo, ni vizuri, ni wazo jema likachukuliwa likafikiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya shilingi milioni 400 ambazo zimepelekwa, Mheshimiwa Mbunge anaomba kwamba ziruhusiwe zihame kwenda kwenye maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ili tuweze kukamilisha kituo cha afya kwa mujibu wa standard, lazima tuwe na uhakika chumba cha upasuaji kipo, wodi ya wazazi kwa maana ya akina mama na watoto, wodi ya akina baba ipo, maabara, nyumba za watumishi za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachowaomba na niziagize halmashauri zote, pale ambapo pesa zimeletwa na Serikali si lazima, eti pesa hiyo iishie hapo, itumike busara kuhakikisha kwamba, kwa utaratibu wa Force Account tunatumia pesa ili ikibaki tukiwa na serving hakuna dhambi ya kuhakikisha kwamba, pesa hizo zinaweza zikahamia kwenda kumaliza matatizo mengine. (Makofi)
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni sera ya Serikali kuwa na hospitali katika ngazi ya Wilaya ili kutoa huduma ya afya kwa wananchi wetu. Wilaya ya Karatu ina umri wa zaidi ya miaka 20 na haina Hospitali ya Wilaya. Ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Karatu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi naomba niziase Halmashauri zote, ni wajibu wetu wa kuhakikisha kwanza tunaanza kwa kutenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za afya, lakini kama hiyo haitoshi, kwa kushirikisha wananchi ni vizuri tukaanza halafu Serikali ikaleta nguvu yake. Ahsante. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kata ya Marangu Magharibi yenye vijiji saba haina zahanati hata moja na hasa vijiji vya Kiraracha na Kitowo wako kwenye hali mbaya sana. Mbunge kwa kushirikiana na wananchi wameweka nguvu zao wanajenga zahanati kwa sasa na imefikia hatua za mwisho.
Nini commitment ya Serikali angalau milioni 20 ya dharura, ili kata hii iweze kupata kituo cha afya cha kisasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika fursa niliyopata ya kutembelea Mkoa wa Kilimanjaro nilijionea. Nilienda Moshi Vijijini nikakutana na wananchi wa Kiafeni, nikakuta kwamba hawakai wakasubiri Serikali ifanye, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge na yeye anakiri na wana utaratibu mzuri, wanasema siku ya utawala wanakwenda kushiriki wananchi kwa ujumla wake. Nguvu ambayo inatolewa na wananchi ukishirikisha na nguvu ya Serikali nina imani hata hiyo kazi ambayo imefanywa na wananchi anaosema Mheshimiwa Mbatia, hakika kwa kutumia uwezo wao wa ndani, kwa maana ya commitment kutoka katika Halmashauri, naomba niitake Halmashauri ihakikishe kwamba wanajibana ili huduma ambayo inahitajika kwa wananchi iweze kufikiwa kwa kumalizia zahanati.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kufuatia majibu ya Mheshimiwa Waziri, ni dhahiri kabisa imeonyesha ni jinsi gani miundombinu ya kujifunzia na kujifunza katika Halmashauri ya Mji wa Tarime hairidhishi na inapelekea matokeo mabaya kwa ufaulu wa wanafunzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wa Tarime wameitikia sana wakishirikiana na wadau mbalimbali ikiwepo mimi mwenyewe Mbunge. Tumejenga madarasa mengi lakini mengi yamekaa bila kuezekwa na kwa kuwa kuna Shule ya Msingi Mtulu ambayo imejengwa na wananchi kwa kujitolea madarasa sita pamoja na ofisi lakini Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji amezuia ile shule wananchi wasiendelee kujenga kwa kile anachokiita kwamba ni mgogoro wa ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sasa kupitia Wizara hii ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais na Rais ana mamlaka ya kubadilisha matumizi ya ardhi, wawatie moyo wananchi wale waliojenga yale madarasa ili sasa waweze kuamuru ile shule iendelezwe ili kupunguza adha ya upungufu wa madarasa katika Halmashauri ya Mji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Halmashauri ya Mji kuna shule moja ambayo inatumiwa na shule tatu, Shule za Msingi Azimio, Mapinduzi na Sabasaba. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kipindi hicho akiwa Naibu Waziri alitembelea sisi kama Halmashauri ya Mji tunataka ile shule ijengwe ghorofa ili sasa walimu wasikae kwenye mti kama Ofisi, wanafunzi wasifundishiwe nje chini ya mti, wanafunzi wasirundikane 120 kwenye darasa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini sasa Serikali isiweze kutumia ile asilimia tano ambayo walisema Waziri anaweza akapeleka kwenye matumizi mbalimbali kama tulivyoona ilivyoenda Chato kwenye uwanja wa ndege. Kwa nini msijenge ghorofa katika shule ile kwenye zile asilimia tano ambazo ni zaidi ya shilingi trilioni 1.7 ili sasa kupunguza adha ya ukosefu wa madarasa katika Mji wa Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema ukisikia upande mmoja, hakika upande ambao haujasikilizwa utakuwa lazima umekosa. Itakuwa ni vizuri tukajiridhisha sababu ambazo zimesababisha Mkurugenzi azuie uendelezaji wa hiyo shule ili tunapokuja kutoa taarifa iwe ni taarifa ambayo iko balanced. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie mbunge, miongoni mwa maeneo ambayo nitatembelea ni pamoja na kwenda kutazama uhalisia wa hiki ambacho nakisema kwa sababu lengo ni kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano wa vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaase Waheshimiwa Wabunge na viongozi kwa ujumla, kwamba katika Wilaya ya Tarime, vijana ambao wanamaliza kuanzia darasa la kwanza mpaka darasa la saba wapo 25,000 lakini vijana ambao wanajiandaa kuingia darasa la kwanza wapo 13,000; kwa hiyo, unaweza ukaona sisi kama taifa kuna mambo ambayo lazima tu-address namna ya population growth inavyokwenda, tukiacha tukatizama hivi tukidhani kwamba Serikali peke yake inaweza hakika haiwezekani. Ni vizuri tukashirikishana pande zote ili kutatua matatizo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya swali lake la pili juu ya ujenzi wa ghorofa, ghorofa jambo zuri na ningependa na mimi nijiridhishe halafu tuone na uwezo wetu maana unapotengeneza chakula lazima ujue na unga upo kiasi gani kwa sisi tunaokula ugali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na juu ya asilimia tano nitaomba niwasiliane na Mheshimiwa Mbunge tuone hiyo asilimia tano na tutayamaliza ili tatizo hili liweze kutatuliwa lakini siamini kwamba asilimia tano inajenga ghorofa. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Tanzania, wanajenga sana zahanati, madarasana mifereji.
Je, Serikali haiwezi kuwa na mpango Maalum kwamba wananchi wakijenga kiasi fulani Serikali nayo inakuwa na kiasi fulani inachukua kumalizia kwa sababu watanzania wanajenga mno? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ni kama amerudia yale ambayo nilikuwa nawaasa Waheshimiwa Wabunge, kwamba hakika kwa kushirikishana wananchi pamoja na Serikali kwa pamoja tunafika na ndiyo maana nikatoa mfano nilivyokuwa nimeenda Moshi Vijijini, Kituo cha Afya ya Kiaseni nimekuta wananchi wamejitoa na Serikali nayo ikapeleka nguvu, hakika tukishirikishana tutaweza kutoka. (Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongza Mheshimiwa Rais kwa utaratibu wa kutoa elimu bure kwani wanufaika wakubwa ni watoto wenye ulemavu ambao siku za nyuma hawakuweza kupata nafasi hiyo. Hata hivyo, pamoja na jitihada hizo, changamoto ndio bado zipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala zima la madawati, madawati ni kweli kabisa yametolewa lakini hayakuzingatia uhitaji hasa kwa watoto wenye ulemavu ambao wengine bado wanalazimika kukaa chini kutokana na hali zao haziwawezeshi kukaa katika madawati hayo.
Je, Serikali ina mpango gani ili basi kuzingatia mahitaji ya watoto hao wenye ulemavu ili waweze kufurahia maisha na kusoma vizuri ili waweze kutimiza ndoto za? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nia thabiti ya Serikali kuhakikisha kwamba makundi yote yanazingatiwa katika kutengeneza miundombinu, na ndiyo maana katika hizi siku za karibuni nilivyopata fursa ya kutembelea Mkoa wa Arusha, nikafika Kituo cha Afya Muriet, pale unakuta miundombinu kwa ajili ya walemavu nayo imewekwa. Naomba niwatake Wakurugenzi wote wa Halmashauri, jambo lolote kuhusiana na miundombinu inapotengenezwa sasa hivi lazima tuhakikishe hitaji la watu maalum.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru sana. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, pamoja na kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali lakini bado kuna changamoto kubwa kwa akina mama wajawazito wanapokwenda hospitali za umma kwa ajili ya kupata vipimo na matibabu mengine, vifaa havipatikani. Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya hili?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali inafanya kazi nzuri sana ya zoezi la ukusanyaji damu salama na imetoa mwongozo mzuri kwa Halmashauri zetu kutenga bajeti kwa ajili ya kukusanya damu salama, lakini bado ziko Halmashauri zimeshindwa kutenga bajeti hiyo. Je, Serikali pia inatoa tamko gani kwenye Halmashauri hizi zilizoshindwa kufanya kazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu katika swali langu la nyongeza na mwenyewe amekiri jitihada kubwa ambazo zinafanywa na Serikali ili kuhakikisha kwamba vifaa tiba vinapatikana na kuondoa adha na hasa kwa akinamama kama ambavyo na yeye mwenyewe amekuwa mdau mkubwa kuhakikisha kwamba akinamama hawapati adha hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee naomba niendelee kupongeza Halmashauri yake ambayo Mheshimiwa Mbunge amekuwa akihakikisha kwamba vifaa tiba vinanunuliwa. Nizitake Halmashauri zingine wahakikishe kwamba vifaa tiba vinatengewa pesa na vinanunuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na Halmashauri yake kwa sababu katika hizi pesa ambazo zimelipwa milioni 41 niliyotaja ni pamoja na kitanda cha upasuaji kimeshalipiwa, mashine ya kutolea dawa ya usingizi, jokofu la kuhifadhia damu kama ambavyo amesema Halmashauri zingine hazifanyi, wao wanafanya vizuri sana; mashine ya kufulia moja, vitanda vya kujifungulia vinne, mfumo wa hewa ya oxygen, vitanda vya kubebea wagonjwa. Kwa hiyo, kwa ujumla nizitake Halmashauri zingine zote nchini waige mfano mzuri ambao wenzetu wanafanya ambako Mheshimiwa Mbunge amesemea.
MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza niishukuru sana Serikali kwa mkakati huo, pia nimshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kutia moyo. Nina swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mkoa wa Geita imekuwa ikihudumia wagonjwa wengi sana kiasi kwamba inaelemewa kabisa. Hii ni kutokana na mapungufu makubwa yaliyopo katika Hospitali zetu za Wilaya. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuweza kuboresha hospitali zetu hizi za Wilaya ili kupunguza msongamano wa wagonjwa uliopo katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Geita? Ahsante.
(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Serikali ina nia njema ya kuhakikisha kwamba, kwanza si kuimarisha Hospitali za Wilaya, tunaanzia kwanza kuimarisha vituo vya afya ndiyo maana pesa nyingi sana imepelekwa ili kupunguza ule msongamano ambao wananchi watalazimika kwenda hospitali ya Wilaya. Kama hilo halitoshi tunajua kabisa, ili kuweza kupunguza mlundikano kwa wananchi ambao wangependa kwenda hospitali za mikoa ni kuwa na uhakika wa kutibiwa katika hospitali za wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwatake wananchi na Halmashauri zetu zote nchini, wahakikishe kwamba, maeneo kwa ajili ya kujenga hospitali za Wilaya yanatengwa kwa kufuata viwango ambavyo vinatakiwa na Halmashauri kwa kutumia own source waanzishe na Serikali itaweka mkono wake. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kulifanyia swali langu kazi ya kutosha. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kutokana na kutenga Sh.253,913,281/= kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya maabara. Je, ni lini fedha hizo zitatolewa kwa sababu, zikichelewa watoto watakuwa wanakosa masomo ya sayansi ki- practical?
Mheshimiwa Spika, swali lingine dogo la pili ni kwamba, kutokana na kutenga shilingi milioni 70 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maabara zile ambazo bado hazijakamilika, ningependa kujua kwa dhati kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, lini fedha hizo zitatoka? Nami naahidi kuwahamasisha wananchi wa Hanang kujitolea kwa kiasi ambacho kimepangwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba, hiki ambacho kimekusudiwa kwa maana ya kununua vifaa vya maabara na kukamilisha maabara inafanyika kwa wakati. Pindi pesa zitakapokuwa zimekamilika kupatikana hakika nimhakikishie Mbunge kwamba, pesa hizo zitapelekwa. Cha msingi tuhakikishe kwamba, zinafanya kazi iliyokusudiwa.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, majibu yake ni sawa na lile la kwanza.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kutokana na Sera nzuri ya Serikali ya CCM ya Elimu Bila Malipo imesababisha mwamko wa elimu na wanafunzi kufauli kwa kiasi kikubwa na kusababisha upungufu wa madarasa zaidi ya vyumba 45 katika Jimbo langu. Je, Serikali imejipangaje katika kutatua tatizo hili la ujenzi wa vyumba 45 ukizingatia kipindi hiki wananchi wengi wako kwenye kilimo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, upungufu wa vyumba vya madarasa ambavyo vipo kwenye jimbo lake, hakika upungufu huu upo kwenye majimbo mengi. Katika moja ya maswali ambayo nilijibu wakati ameuliza Mheshimiwa Esther Matiko akiwa anaongelea juu ya uhaba wa vyumba vya madarasa, nika- refer kwamba, ni wajibu wetu sisi wananchi kwa kushirikiana na sisi viongozi pamoja na Serikali, kwanza kwa kutazama idadi ya vijana ambao wanajiunga na shule zetu na hasa baada ya mwitikio mkubwa baada ya Elimu Bila Malipo, Sera ambayo inatekelezwa vizuri sana na CCM.
Mheshimiwa Spika, ni wajibu wetu sisi kwa kushirikiana na wananchi tuhakikishe kwamba, kwanza halmashauri zetu ndani ya own source zetu tunatenga na tuwashirikishe wananchi na Serikali nayo itaunga mkono.
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa, mkandarasi anaendelea na mkataba mpaka kuezeka. Je, Serikali ina mpango gani wa ku-lease fedha ambazo zitahitajika, ili halmashauri isikiuke mkataba?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa, hatua ya kuezeka inakwenda kukamilika na jengo hili limechukua muda mrefu. Je, Serikali iko tayari kutenga fedha kwa mwaka ujao wa fedha, fedha za kutosha ili kukamilisha jengo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba kandarasi zote ambazo zimeanzishwa hatuishii njiani. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie na nimwombe mkandarasi aliyepo hapo aendelee na kazi ili pesa ambayo imeahidiwa na Serikali ikifika asilazimike kwamba awe ametoka site na kulazimika kurudi kwa mara nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kwa kushirikiana na Mbunge na nia njema ya Serikali kuhakikisha kwamba katika bajeti 2018/2019, ujenzi huu unaendelea, kwa hiyo tuweke kwenye bajeti.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake ambayo yametoa matumaini kwamba watafanyia research udongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi, Jimbo la Igunga ni Jimbo ambalo udongo wake hauwezi kujengwa kwa kukwangua barabara lazima uweke tuta kwahiyo hela zinazotengwa kwa Halmashauri hizi hazitoshi kabisa kujenga hizi barabara.
Swali la kwanza, je, kwa nini Serikali isilete upendeleo kwenye Jimbo hili la Igunga ikasaidia kujenga barabara za vijijini?
Swa li la pili, kwa azma ya Serikali ya kuunganisha Mikoa Tanzania, kwanini Serikali isijenge kwa kiwango cha lami barabara inayotoka Kolandoto kupitia Igurubi kwenda Igunga, Mbutu na kwenda mpaka Loya kwenye Jimbo la Igalula na mpaka Tura kwenye barabara ya lami itokayo Tabora kwenda Dodoma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo swali lake la msingi linaeleleza jinsi ambavyo eneo lile linahitaji kutazamwa kwa umakini kwani udongo ule ni tofauti na maeneo mengine.
Kwanza naomba nikubaliane naye kwamba siyo kama suala la upendeleo lakini ni vizuri tutakatazama kulingana na hali ya barabara zile na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, essence ya kuanzia TARURA, Waheshimiwa Wabunge wengi tumekuwa ni mashahidi hapa tumekuwa tukiomba barabara zetu zipandishwe hadhi zichukuliwe na TANROADS kwasababu tukiamini TANROADS inafanya kazi vizuri zaidi. Naamini kwa kuanzishwa kwa chombo hiki cha TARURA hakika barabara zetu zitatengenezwa katika kiwango ambacho kitakuwa bora zaidi. Naamini na barabara hii ya Mheshimiwa Kafumu nayo kwa kupitia TARURA na kwa sababu inahitaji kiasi kingi che fedha, fedha ambayo itatengwa na Serikali itakuwa nyingi ili kuweza kukidhi hali ya barabara hiyo.
Kuhusiana na swali lake la pili la kuunganisha barabara kutoka Kolandoto mpaka Tura ambayo kimsingi jiografia yake inaonyesha ni kwamba itakuwa ni kiungo kikubwa sana mpaka kufika Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kama Serikali tulichukue, tulifanyie kazi halafu tuone namna itakayokuwa bora katika kulitekeleza.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza.
Kwa kuwa mgao wa Road Fund Serikali Kuu wanachukua asilimia 70 na Serikali za Mitaa asilimia 30 na kwa kuwa Serikali imeunda chombo cha TARURA na kama mgao utakuwa asilimia 30 zile zile na barabara zetu ni mbaya sana vijijini kule hasa Wilaya ya Mpwapwa.
Je, sasa mgao utaongezeka iwe asilimia 50 kwa 50?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi asilimia 70 na asilimia 30 ni kwa mujibu wa Sheria na Sheria hii ilitungwa na Bunge lako Tukufu. Kama haja itakuwepo kwa wakati huo tutakubaliana kiasi gani ambacho kitafaa na lengo ni kuhakikisha kwamba chombo hiki ambacho tumekianzisha TARURA kinakuwa na uwezo ili kiweze kukidhi haja iliyoanzishwa.
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambazo ziko kwenye Mji mdogo wa Sirari na Mji mdogo wa Nyamongo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais akiwa pale na ziko TARURA.
Unasemaje kuhusu kutupa angalau kilometa mbili za lami ili kuondoa matatizo kwenye Mji ule ambao una watu wengi Miji miwili hii ambayo ni Sirari na Nyamongo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi za Mheshimiwa Rais zimetolewa maeneno mengi na sisi sote ni mashuhuda kwamba tumeletewa taarifa kwamba uratibu utafanyika kuhusiana na ahadi zote ambzo zilitolewa na Mheshimiwa Rais na kimsingi katika kutekeleza ahadi hizo tunahitaji miaka mitano, ndani ya miaka mitano tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba ahadi za Rais zinatekelezwa naamini katika kipindi hicho na eneo lake litatekelezwa kwa kujengewa hiyo barabara ya lami.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyingeza, lakini kabla ya hapo naomba uniruhusu kwa kifupi sana nimshukuru Naibu Waziri Mheshimiwa Kandege alifika Urambo na kujionea mwenyewe, ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri, karibu tena, ulifanya kazi nzuri na kusababisha tupate wafanyakazi 17 kama ulivyosema lakini sasa swali la nyongeza ni kama ifuatavyo:-
Kwa kuwa Serikali imeona uhaba wa wafanyakazi uliopo na kutokana na wagonjwa wengi kutoka jirani zangu Kaliua ambako hawa Hospitali ya Wilaya wakiwemo kutoka Ulyankulu, Uyui, Uvinza. Naomba kuwauliza Serikali kama wako tayari kuongeza wafanyakazi ili tuendelee kutoa huduma nzuri?
Swali la pili ni kwamba, kutokana na ongezeko la wagonjwa wengi kutoka Kaliua, Uyui, Uvinza ikiwemo Ulyankulu, je, Serikali iko tayari kutuongezea fedha ikiwemo fedha za Busket Fund ili tuweze kumudu ongezeko la wagonjwa ambao wanatoka jirani? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba wa dhati nipokee pongezi kutoka kwa Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta.
Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi tulifanya ziara kule na tukajionea kazi nzuri ambayo naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana jinsi ambavyo anahangaika na suala zima la afya za wananchi wa Urambo na tulipata fursa ya kutembelea Hospitali ya Wilaya na katika moja ya ombi ambalo Mheshimiwa Mbunge aliwasilishwa kwetu Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni pamoja na suala zima la kubadilishiwa matumizi kiasi cha shilingi milioni 150 ili ziweze kutumika katika kujenga wodi ambayo ni Grade A wazo ambalo tumelichukua na punde tutalifanyia kazi ataweza kupata majibu ili pesa ile iweze kutumika.
Kuhusiana na suala zima la uhitaji wa watumishi ili kukidhi haja ya wagonjwa ambao wanasafiri kutoka Wilaya nyingine kwenda Wilaya ya Urambo kwanza naendelea kumpongeza, ukiona wagonjwa wanakuja kwako maana yake huduma ambayo inatolewa na hospitali yako ni nzuri ukilinganisha na wengine.
Kwa nia hiyo hiyo njema na katika kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Urambo, wewe ni shuhuda tulikubaliana, jitihada zinafanywa na Serikali hivi karibuni pesa zitakuja kwa ajili ya kulimalizia ile wodi ambayo ilikuwa imeanzishwa kutoka Wizara ya Afya.
Lakini kama hilo halitoshi, naomba niungane mkono kabisa na Mheshimiwa Magret Simwanza Sitta kwamba iko haja ya kutazama kwa kadri nafasi itakavyoruhusu watumishi wakipatikana ili kuweza kuongeza maana ukienda Kituo cha Afya Usoke pale tumeona kazi nzuri ambayo inafanyika na itakamilika hivi karibuni iko haja ya kuongeza watumishi pale watakapokuwa wamepatikana.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO:Mheshimiwa Naibu Spika,asante kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi kwamba ukosefu wa makazi bora ya walimu kunawakatisha tamaa walimu kuishi vijijini na mara kwa mara walimu wengi wamependa kuhama kutoka kwenye maeneo haya na kuhamia maeneo ya mijini ambako kuna makazi bora. Ukichukulia Halmashauri moja tu ya Tunduru mahitaji ni nyumba za walimu 1782; upungufu 1688 lakini Naibu waziri amesema ana mpango wa kujenga nyumba 30 katika mkoa mzima wa Ruvuma naona hii kasi ni ndogo nilipenda kujua Serikali ina mkakati gani katika kuhakikisha jambo hili tunalimaliza kwa haraka na ukizingitia sisi wote tumetokana na hao walimu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba ni wajibu wetu sisi Serikali Kuu Halmashauri pamoja na wananchi kwa ujumla tukizingatia kwamba upungufu huu ni mkubwa sana haitakuwa busara tukasema tunaiachia Serikali peke yake, tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba tunashirikishana ili tatizo hili tulimalizekwa haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, na hii naomba nirejee kwa ruhusa yako jana wakati Mheshimiwa Gekul wakati anaomba Mwongozo kwa Mheshimiwa Spika alisema kwamba kuna barua (Waraka ambao umetolewa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI) ukiwataka wananchi kwamba kuanzia sasa hivi ni wajibu kushiriki kuanzia mwanzo kwa maana ya msingi hadi kwenda kumalizia. Kabla Serikali haijaleta taarifa yake rasmi naomba niseme kwamba hakuna waraka kama huo ambao umepelekwa ni wajibu wetu sisi wananchi pamoja na Serikali kushirikiana ili kumaliza matatizo yanayohusu watumishi wa Serikali.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza awali ya yote sina budi kushukuru kwamba hali ya ulinzi Kibiti inazidi kuimarika. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kumshukuru Rais wetu, kipenzi chetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Kibiti sasa kinazidiwa, je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha ili kuwa Hospitali ya Wilaya ya Kibiti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba hospitali inazidiwa na tafsiri yake nini ambacho kinatakiwa kufanyika? Ni kwamba tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya vingi ili Hospitali ya Wilaya hiyo iwe na sehemu ya kupumulia.
Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu Mheshimiwa Mbunge awahimize wananchi wake waonyeshe nia ya kuanza ujenzi na Serikali itapeleka mkono pale ambapo tayari wananchi washaanza ujenzi.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi napenda niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini na Halmashauri ya Mji ya Bunda Mjini wanataka Hospitali ya Manyamanyama iwe Hospitali ya Wilaya na tayari vikao vya Halmashauri vilishakaa. Tatizo hawana jengo la mortuary na tayari kupitia wadau wameshaanza ujenzi. Je, Serikali haioni kwamba inapaswa kuisaidia Halmashauri ya Mji wa Bunda na hasa ukizingatia Halmashauri ile ni changa kumaliza jengo lile ili sasa ile dhamira ya Hospitali ya Manyamanyama kuwa hospitali ya Wilaya ifanikiwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nilipata manufaa na faida ya kwenda kutembelea Halmashauri ya Bunda nikiwa na ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na kwa bahati mbaya Mheshimiwa Mbunge hakuwepo, angekuwepo tungeenda Manyamanyama tukapata fursa ya kujua nini hasa ambacho kinatakiwa kifanywe ili tuweze kushirikiana. Naomba kwa wakati mwingine tuungane tuone namna nzuri ya kuweza kusaidia ili wananchi waweze kupata huduma.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kutokana na jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri inaonesha kabisa kuna upungufu mkubwa wa watumishi 240. Katika mwaka 2017 wameajiri watu 22 vilevile mwaka ujao wanapanga kuajiri watu 121, hii inaonesha ni mkakati wa kawaida tu na kwa sababu hiyo hawajaweza kukidhi kile ambacho mimi nilikuwa nahitaji kujua. Mimi ninachotaka kujua, ni lini sasa Serikali itakuwa na mkakati wa dharura wa kuhakikisha kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Geita inapata watumishi wa kutosha ili waweze kuwapatia wananchi huduma inayostahiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika Halmshauri ya Wilaya ya Geita hasa katika Jimbo la Busanda kuna baadhi ya vituo vya afya ambavyo kwa kweli vina upungufu mkubwa sana hasa katika Kituo cha Afya Katoro ambapo kuna idadi kubwa ya watu vilevile kituo hicho kinahudumia pia na Kata zingine jirani kama Rwamgasa, Busanda pamoja na Kasemye. Kitu hiki kina upungufu mkubwa sana wa wataalam kiasi kwamba inasababisha hata wakati mwingine watu kupoteza maisha yao. Ni lini sasa Serikali itahakikisha inapeleka watumishi kwa dharura katika kituo hiki cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza anauliza mkakati wa dharura, ni ukweli usiopingika kama tulivyokiri kwenye jibu letu kwamba upo upungufu mkubwa sana na namna pekee ni kuweza kuajiri na suala la kuajiri ni pamoja na bajeti inaporuhusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi tukubaliane kwamba kwa kuanzia na hao ambao tumewataja 121 si haba na kwa sababu katika majibu yangu kwenye swali la msingi nimemueleza sababu zilizosababisha upungufu huu mkubwa, siyo rahisi kwamba kwa mara moja tutaweza kuziba pengo hili kwa sababu suala lenyewe lina budget implication.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba Katoro pale idadi ya watu ni kubwa na iko haja ya kuhakikisha kwamba pamoja na hospitali iliyopo vijengwe na vituo vingine vya afya ili kuweza kuongeza maeneo ya afya kuweza kutibiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kwa kupitia Halmashauri yake wana uwezo wa kuweza kufanya allocation ndani kutazama maeneo yapi ambayo staff wako wengi ili ndani kwa ndani kwanza kupunguza wakati wanasubiri ajira kutoka Serikali kuu. (Makofi)
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Halmshauri ya Kaliua ina upungufu wa watumishi kwa asilimia 76, waliopo ni asilimia 24 tu. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, kuna mkakati gani wa dharura kuhakikisha kwamba angalau kwa Kaliua kabla hata ya kuandika barua maana nasema hapa wanapatiwa watumishi wa afya ili akina mama waache kuteseka kwa kukosa huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):Mheshimiwa Naibu Spika, umenisaidia kwa sababu majibu aliyotoa Mheshimiwa Waziri wa Nchi na Mheshimiwa Sakaya yuko hapa, sidhani kama itakuchukua muda mrefu kuandika barua kuainisha huo upungufu ili hili jambo liweze kufanyiwa kazi kwa mara moja.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza nifanye marekebisho kidogo kwenye majibu, hili Daraja la Mongolandege lipo kwenye Mto Msimbazi sio Mto Mzinga, lakini vilevile kwa majibu haya, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa sababu Serikali inakiri kwamba mvua ilinyesha ikaleta madhara makubwa na Daraja la Mongolandege na Mto Nyebulu unatenga maeneo mawili tofauti kwenye huduma za jamii yaani upande mmoja ndiyo kuna shule ya sekondari, msingi, afya na huduma zote za kijamii na upande mwingine wananchi wanakaa pale. Katika hali hiyo mvua ikinyesha huwa ni kisiwa, wanafunzi hawaendi shule mpaka mvua iishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua ni kwa nini Serikali isijitahidi mwaka huu wa fedha ifanye usanifu na fedha itengwe kwa ajili ya kazi hii? Maana kwenye majibu yake anasema wataangalia na baadaye bajeti itengwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa sababu eneo hili ni muhimu na wananchi wanapata shida, tunaweza kupata huduma ya dharura ya daraja la muda katika maeneo yote mawili ili huduma ziendelee hasa wakati wa mvua tunapoelekea mwezi Aprili? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, uwezekano wa kuweza kutenga fedha kipindi hiki ambacho bajeti tayari imeshapitishwa na Bunge lako Tukufu jambo hili litakuwa na ukakasi mkubwa sana. Tutakubaliana na Mheshimiwa Waitara kwamba ili daraja hili liweze kujengwa kwa kina lazima usanifu ufanyike ili isije ikatokea kama yale yaliyotokea mwanzo.
Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba Mheshimiwa Mbunge avute subira na leo nilikuwa nafanya mawasiliano na TARURA, kwa kuanzia kwa ajili ya usanifu itatengwa jumla ya shilingi milioni 100 na ujenzi kwa ajili ya kuanza, tutatenga jumla ya shilingi milioni 300. Kwa hiyo, asipate shida, naomba nimhakikishie kwamba jambo hili liko kwenye mikono salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya suala la daraja la dharura. Ni wazo jema, ni vizuri tukajua wapi tunaweza tukalipata daraja la muda, lakini baada ya kwenda site kutazama uhalisia wa jambo lenyewe likoje. Kwa sababu huwezi ukasema daraja la muda linafananaje bila kwenda site kujua uhalisia ukoje. Nashukuru.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina swali la nyongeza. Serikali iko moja nayo ni Serikali Kuu na hao wote waliotamkwa wanatekeleza kutokana na maagizo ya Serikali Kuu. Je, inakuwaje pale ambapo hela hazipelekwi za kutosha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali inafuatilia vipi kuepusha migongano hiyo kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pale ambapo fedha za kutekeleza mradi fulani hazijapelekwa zote mawasiliano yanafahamika kati ya waliopokea na waliopeleka. Kwa hiyo hayo yanakuwa ni maelezo sahihi wakati wa tathmini kwamba hatukuweza kutekeleza vizuri mradi huu au hatukukamilisha kwa sababu fedha imekuja nusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hiyo ni mawasiliano ya ndani ya Serikali na mara nyingi imefanyika; lakini kitu kimoja kizuri kwa upande wa Serikali za Mitaa ni kwamba wanapopewa wakati mwingine fedha imezidi au imechelewa kuja imekuja mwishoni mwa mwaka wa fedha wenzetu wanaruhusiwa kubaki na fedha ile halafu mwezi wa Saba wanakaa kwenye vikao vyao rasmi wanazipitisha kwa ajili ya matumizi yaliyovuka mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili kwamba tunafuatiliaje mgogoro; Serikali ina macho usiku na mchana. Kule kule ziliko Serikali za Mitaa wapo waangalizi wa Serikali ambao wanakusanya taarifa kila siku asubuhi na mchana kwa masaa yote. Kwa hiyo kama kuna harufu yoyote ya mgogoro Serikali Kuu huwa inapata taarifa hizo mara moja. Ahsante sana.
MHE. MAIDA H. ABDALLAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa miradi mingi ya maendeleo ngazi ya Halmashauri imekuwa ikisuasua na ikikwama kutokana na ucheleweshwaji wa fedha kutoka Hazina. Je, Serikali inatoa kauli gani katika ukamilishwaji wa miradi ya maendeleo iliyopitishwa na bajeti ya Serikali mwaka 2015/2016 na 2016/ 2017?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kusuasua kwa miradi; huku kunategemea na eneo na mradi na Halmashauri husika. Ziko Halmashauri ambazo tumekuwa tukizifuatilia na kuwashauri kuhusu matumizi ya fedha kwa wakati. Wakati mwingine wanakuwa na fedha kwenye akaunti lakini wakati mwingine watekelezaji kule kwenye mradi wanakuwa hawajui kama fedha zimekuja. Kwa hiyo matatizo mengine ni ya kimawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusisitiza, Halmashauri mara zinapopata fedha kutoka Serikali Kuu, zijipange kwa haraka na kwa wakati kutumia fedha hizo kwa ajili ya wananchi, wasiziache kwenye akaunti. Pale ambapo kuna ucheleweshaji wa aina yoyote wafanye mawasiliano haraka na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kusudi tuweze kufuatilia kwa wenzetu tuweze kusuluhisha suala hilo mara moja.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Baadhi ya Wakuu wa Wilaya na Mikoa hapa nchini wamekuwa wakiwasimamisha hovyo watumishi wa Serikali za Mitaa bila kufuata taratibu na sheria zilizopo. Je, nini kauli na msimamo wa Serikali katika suala hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kukanusha, hakuna sehemu yoyote ambayo Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa amesimamisha watu kazi hovyo, hakuna! Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba usimamishaji wowote wa kazi unafuata masharti ya taratibu za kazi na sheria zinazomwongoza anayetoa amri hiyo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Maagizo yaliyotolewa na Serikali ya kuhamishia watoto wenye uhitaji wa elimu maalum ifikapo Desemba 31 mwaka huu hayatekelezeki; kwa sababu hata kwangu Wilaya ya Kakonko hakuna shule hiyo. Swali la kwanza, Serikali iko tayari kujenga shule ya watoto wenye uhitaji wa elimu maalum katika Wilaya ya Kakonko ikizingatiwa kwamba kuna watoto zaidi ya 200, Walimu wako watano tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa maelezo hayo hayo ambayo nchi nzima itaathiriwa na agizo hili la Serikali, je, Serikali inaweza ikajiridhisha kwamba kila wilaya inapata shule ya watoto wenye vipaji maalum yenye mabweni ili kuwaokoa katika usumbufu wanaoupata? Ahsante.
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, hajasahau taaluma yake licha ya kuwa Mbunge. Sasa naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kasuku kama ifuatavyo:-
Serikali imeshatoa maagizo tangu mwaka jana kwamba kila halmashauri iteue shule angalau moja ili watoto wenye mahitaji maalum waweze kusomeshwa vizuri kwa mujibu wa mazingira ya mahitaji yao. Sasa kama kwenye wilaya yake hakuna hata shule moja, natoa agizo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo ili aweze kutekeleza agizo la Serikali lililotolewa tangu mwaka jana mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, amezungumza kwamba kwenye eneo lake la Ubunge wapo Walimu watano tu ambao wana taaluma ya elimu maalum. Namhakikishia kwa agizo ambalo limetolewa na Serikali leo; mimi nimesisitiza tu lilishatolewa siku nyingi, nasisitiza na kuwapa muda kwamba ifikapo Desemba 31, 2018 agizo hili linatekelezeka. Ndiyo maana tumewapa muda mrefu vinginevyo tungeweza kuwapa mwisho tarehe 30 mwezi wa Juni, lakini tumewapa muda mrefu hadi Desemba ya 2018 ili Halmashauri ziweze kujipanga vizuri kuhakikisha agizo linatekelezeka. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ni kweli baadhi ya halmashauri zimetekeleza agizo la Serikali la kutenga shule moja kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum, lakini ni kweli pia kwamba shule hizi hazina vitendea kazi pamoja na Walimu wa kutosha na matokeo yake hata ufaulu wa watoto umekuwa ukitia shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano Shule ya Sekondari ya Viziwi Njombe ambayo matokeo ya Form Four ya mwaka uliopita shule nzima wamepata division zero. Sasa je, Serikali iko tayari pamoja na agizo hili kuhakikisha kwamba shule hizi zimepata Walimu wa kutosha na vitendea kazi ili hawa watoto waweze kuangaliwa kwa uzito ule ule wa watoto wengine ambao hawana mahitaji kama hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru amerejea kauli yangu kwamba agizo hili la kila Halmashauri kuwa na angalau shule moja ambayo watasoma watoto wenye mahitaji maalum. Napenda kumhakikishia kwamba agizo lile lililotolewa tangu mwaka jana lilienda sambamba na maagizo kwamba wahakikishe shule hizo zinakuwa na vifaa na vitendea kazi pamoja na Walimu ambao watawafundisha watoto hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wake wa Njombe alioutoa, namwagiza Mkurugenzi wa Elimu pale ofisini kwangu afuatilie hiyo shule ya Njombe kuona je, ni ukosefu wa vifaa au ukosefu wa Walimu au ni tatizo la wanafunzi wenyewe lililosababisha wote wapate division zero? Hata hivyo, tunafuatilia na naagiza kwamba kila Halmashauri inapoteua shule ya watoto wenye mahitaji maalum wahakikishe kwamba kunakuwa na vifaa vya kutosha vya kuwafundishia. Ndiyo maana tunaita ni mahitaji maalum kwa sababu mtu ambaye ana ulemavu wa macho anahitaji vifaa maalum vya kusomea. Mtu ambaye ana ulemavu wa akili anahitaji vifaa malum vya kusomea. Kwa hiyo wahakikishe vifaa vyote vinapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni wakati wa kupanga bajeti, kwa hiyo wahakikishe kwamba ikifika mwezi wa Saba tarehe moja, utekelezaji uanze kufanyika kwa mujibu wa maelezo ya Serikali. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo taarifa kwamba wako Walimu wa kufundisha shule za walemavu wamehitimu hawajaajiriwa bado. Tumefanya mazungumzo na Ofisi ya Waziri Mkuu, nimezungumza na Naibu Waziri anayeshughulika na walemavu, tuletewe orodha ya mahitaji ya Walimu kwa ajili shule za walemavu, tutapata kutoka Wizarani orodha ya wale ambao tayari wamehitimu. Tutawaajiri mara moja ili wanafunzi hao nao wapate elimu kama wanafunzi wengine. (Makofi)
MHE. DESUDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na nichukue nafasi hii kutambua juhudi kubwa sana na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri waliyoifanya kwenye shule hii, lakini pia usimamizi mzuri uliotolewa na Mkuu wetu wa Wilaya na kwa hakika nimeridhika sana na majibu ya Serikali, lakini hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; shule hii ni ya bweni kwa kidato cha tano na cha sita. Haina nyumba ya matron wala haina uzio wa ulinzi wa wanafunzi. Naomba Serikali itoe hela zaidi kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na huduma ya vijana hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Halmashauri ilijitahidi kuchimba kisima cha maji lakini kiko mbali kidogo na shule. Naomba Serikali itoe pesa zaidi kwa ajili ya kusogeza maji kwa ajili ya huduma ya wanafunzi hawa. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Mipata na Mheshimiwa Keissy, wilaya yao ni miongoni mwa wilaya zinazoongoza katika ujenzi wa madarasa. Mwaka jana peke yake wamejenga madarasa 550 ambayo yanatakiwa kuezekwa sasa hivi. Kwa hiyo nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili hitaji la kwanza alilosema la nyumba ya matron, uzio; nilifika pale Milundikwa, nimeona kweli ni mahitaji halisi nayo tutayafikiri kadri ambavyo tunapata uwezo wa kifedha lakini kwa kushirikiana na halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu kisima, shule ya sekondari ya Milundikwa tumeiingiza kwenye orodha ya shule 100 ambazo zitapata ufadhili wa fedha kutoka kwa Sultan Qaboos wa Oman. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Tunduma ni mji unaokuwa sana na una msongamano mkubwa sana wa watoto; na mwaka wa jana Waheshimiwa Madiwani kwa kushirikiana na wananchi waliweza kuanzisha shule mpya nane ambazo zingine zina madarasa matatu, zingine zina madarasa nane lakini shule hizi mpaka sasa hivi hazijaanza kutumika kwa sababu DC amewasimamisha Madiwani. Kwa, hiyo kuna baadhi ya shughuli ambazo zilitakiwa zifanyike kama vioo na mambo mengine hayajafanyika kwa sababu wananchi pia walikuwa wanategemea Madiwani. Je, ni lini Serikali itatia mkazo kuhakikisha kwamba Madiwani wanarudi kazini ili shule hizi zianze kutumika haraka iwezekanavyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ilijitahidi ikajenga shule nane na hizi shule hazijaanza kutumika, ni kweli; lakini ni matokeo ya migogoro ambayo haina sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wenzetu wa Halmasahuri ya Mji wa Tunduma walipokaa kwenye kikao cha rasmi walikataa ushirikiano wa aina yoyote na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya. Sasa hilo likawa ni chanzo cha matatizo ambayo yamesababisha Waheshimiwa Madiwani wasiweze kutimiza majukumu yao. Suala lao tunalishughulikia kitaifa na namwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutalitatua hivi karibuni, ili kusudi waweze kuendelea kutekeleza majukumu yao kama kawaida. (Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hospitali ya Manispaa ya Mpanda kwa sasa hivi inafanya kazi kama Hospitali ya Mkoa, imeelemewa kwa kiasi kikubwa na wangonjwa wanaotoka katika Halmashauri mbalimbali. Wakati tukisubiri mipango ya Serikali ya kutujengea Hospitali ya Mkoa, ni lini Serikali itatusaidia kuongeza waganga pamoja na wauguzi? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tuna upungufu wa wauguzi pamoja na madakatari. Nizitake Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda pamoja na Halmashauri zingine waige mfano mzuri ambao umefanywa na Halmashauri ya Handeni kwa kutumia own source ili kuweza kuwaajiri wale watumishi ambao ni muhimu sana kwa kipindi hiki wakati wanasubiri wale ambao wataajiriwa na Serikali.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tatizo lililopo Handeni linafanana kabisa na tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora ya Kitete, ina upungufu mkubwa wa madaktari na wauguzi. Je, ni lini Serikali itapeleka madaktari na wauguzi katika Hospitali ya Mkoa ambayo inategemewa na mkoa mzima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la swali la msingi, ni kweli tunatambua kuna upungufu mkubwa wa wauguzi pamoja na madaktari na hasa katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, kwa kadri ambavyo ikama inahitajika kutokana na bajeti, ni vizuri basi niwatake Mkoa wa Tabora kwa ujumla wake waanze kwa haraka kuiga mfano mzuri wa Handeni kwa kutumia own source za kwao ili kuweza kuziba hilo pengo lililopo wakati tunasubiri bajeti iruhusu kwa ajili ya kuajiri hao wengine ambao watatoka Serikali Kuu. (Makofi)
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza naomba nimpongeze sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kuridhisha. Pia nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali yetu kwa kuipandisha hadhi Hospitali ya Haydom kuwa Hospitali ya Rufaa Ngazi ya Mkoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na upandishwaji hadhi huko, ni kwa nini Serikali yetu isione umuhimu wa kuhakikisha kwamba inajenga miundombinu ya hospitali hii muhimu inayohudumia mikoa zaidi ya mitatu hasa katika suala la upatikanaji wa maji, jambo ambalo ni muhimu sana? Amekiri mwenyewe kwamba source ya maji sasa hivi ni umbali wa kilometa 25 kutoka hospitali kwa kutumia jenereta ambayo inakabiliwa na uharibifu wa mara kwa mara. Suala la REA Awamu ya Tatu linachukua muda mrefu, tungeomba Serikali ifikirie kupeleka umeme katika hospitali hii muhimu kabla ya hata REA kufikia eneo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, suala la income tax kwenye posho za watumishi wa Hospitali ya Haydom tayari ameshaonyesha kwamba kuna tabaka mbili ya watumishi katika hospitali hiyo, lakini ukweli na utafiti unaonyesha kwamba baadhi ya watumishi katika Hospitali za Wilaya na kwingineko katika nchi yetu hawakatwi kodi kwenye on-call allowances lakini hawa watumishi wa Haydom wanakatwa na hasa tukizingatia kwamba wanafanya kazi katika mazingira magumu sana. Tunaomba Serikali itoe kauli katika hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Umbulla, naomba kwa moyo wa dhati kabisa nimpongeze kwa jinsi ambavyo amekuwa akipigania wananchi wa mkoa wake lakini bila kusahau hata Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo jinsi ambavyo wamekuwa wakiipigania hospitali yao hii ya Haydom. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake ya nyongeza anasema kwamba ufanyike utaratibu wa haraka ili kuwezesha kupatikana umeme kabla ya REA.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, utaratibu wa haraka kabisa na chanzo cha uhakika ni kwa kutumia REA Awamu ya Tatu, nadhani ndiyo njia sahihi. Kwa taarifa tulizonazo Serikalini ni kwamba tayari mkandarasi yupo kule. Kwa hiyo, tuvute subira, kama mmesubiri muda wa kutosha, kipindi kilichobaki ni kifupi na tatizo hili litakuwa limeondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na watumishi ambao wameajiriwa na Hospitali hii ya Haydom kukatwa on-call allowance. On-call allowance inakatwa kwa sababu wao katika malipo ambayo wanafanya, wanajumuisha pamoja na mshahara wao na ukisoma ile Sheria ya Income Tax, unapotaka kukata kodi lazima utizame vyanzo vyote, ni tofauti na hawa wa Serikalini ambao allowance hizi huwa zinalipwa dirishani, hazisubiri mpaka kipindi cha kuja kulipa mshahara wa mwisho. Kwa hiyo, ni namna tu watakavyojipanga wakaji-adjust inawezekana kabisa wasikatwe hicho wanachokatwa. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona na namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa majibu yake kwa maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni vizuri tuweke rekodi sawasawa. Bunge hili kupitia Finance Act ya mwaka 2011 liliongeza misamaha kwa posho mbalimbali. Katika vitu vilivyoongezwa kwamba vitasamehewa kodi ya mapato ni allowance payable to an employee who offers intramural private services to patients in a public hospital and housing allowance, transport allowance, responsibility allowance, extra duty allowance and honoraria payable to an employee of the Government or its institution whose budget is fully or substantially paid out of Government budget subvention. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, allowances hizi ndizo zilizosamehewa kodi kwa mujibu wa sheria na TRA hiki ndicho wanachofanya. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tunapozungumza Hospitali ya Amana imepelekwa katika Wizara ya Afya na kwa maana hiyo Manispaa ya Ilala haina Hospitali ya Wilaya. Bahati nzuri katika Jimbo la Ukonga, Kata ya Kivule kuna eneo la ekari 45, Manispaa ya Ilala imeshaanza kuweka msingi.
Je, ili kupata huduma ya afya katika Manispaa ya Ilala kwa kuwa na Hospitali ya Wilaya, nini kauli ya Serikali katika jambo hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Hospitali ya Amana imechukuliwa na hivyo kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge hawana hospitali. Pia ni ukweli usiopingika kwamba jana nilipata fursa ya kuteta na Mheshimiwa Mbunge akaniambia katika own source yao walikuwa wametenga shilingi bilioni moja kwa ajili la kuanza ujenzi wa hospitali yao. Kwa hiyo, ninachowaomba, zile jitihada ambazo walishazianzisha za kuanza kujenga hospitali ya kwao ya Wilaya zisisimame, ni lazima zitiwe msukumo tuhakikishe kwamba wananchi wetu wanapata maeneo mengi ya kujitibia. Nikitoka hapa nitafanya kila jitihada niwasiliane na Mkurugenzi ili nimuelekeze hicho kiasi cha pesa ambacho kimetengwa kifanye kazi iliyokusudiwa.
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wabheja sana. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Jimbo la Kishapu lina zahanati 45 zilizokamilika na zinafanya kazi, vituo vya afya vinne vimekamilika vinafanya kazi na viwili tayari tunasubiri vianze kufanya kazi hivi karibuni na tuna hospitali kubwa ya kisasa ambayo inafanya kazi vizuri. Kwa kuwa tumekwishaleta maombi ya upungufu wa baadhi ya madaktari, wauguzi na watumishi wa kada ya afya, je, Mheshimiwa Naibu Waziri, uko tayari kukaa na mimi hata leo tupitie maombi hayo uone namna ambavyo utasaidia jitihada za watu wa Kishapu? Mheshimiwa Mwenyekiti, wabheja sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabla ya kujibu kama niko tayari au siko tayari, naomba niwapongeze kwa jitihada ambazo zimefanyika za kuweza kuhakikisha kwamba huduma za afya zinapatikana kwa kiwango kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niko tayari kabisa, kabisa. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa muda wa kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali hii ya Haydom kwenye swali la msingi iko katika jimbo langu na inaihudumia Mikoa ya Arusha, Manyara, Mara, Singida na Shinyanga. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu alishafika na kutuahidi kwamba atatupatia watumishi zaidi na Mheshimiwa Ummy amefika kwenye hospitali hiyo. Je, lini sasa Serikali inatimiza ile ahadi yake ya kutupatia watumishi katika hospitali hii ambayo inahudumia mikoa mingi niliyoisema?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilishatoa ahadi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tatizo la watumishi linaweza kutatuliwa haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mbunge ni shahidi, jana alikuwepo, Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora alitoa majibu kwamba kwa zile Halmashauri na maeneo ambayo tunahitaji kuweza kuziba pengo hilo kwa haraka ni vizuri barua zikaandikwa. Pia tunakiri kabisa juu ya kujengea uwezo Hospitali ya Haydom kwa sababu inahudumia wagonjwa wengi, naomba tufuate procedures za kawaida ili jambo hili liweze kutatuliwa kwa wakati.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nitoe shukrani kwa Serikali, wanasema kwamba usiposhukuru kwa kidogo basi hata kikubwa hutaweza kupata, kwa sababu nililalamika hapa sina hata kituo cha afya kimoja, lakini sasa hivi nimepewa pesa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha pili na pesa za kuboresha kile kituo cha afya cha zamani ambacho nilisema ni mfu, kwa hiyo nasema ahsanteni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado Hospitali ya Wilaya ya Liwale ina tatizo la nursing officers na mpiga picha wa x-ray. Ni lini Serikali itaweza kutupatia watumishi hawa wa kada mbili; mpiga picha wa x-ray na nursing officers? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Liwale, ambalo kimsingi amekuwa akipigania sana wananchi wake na mimi najua na jana alikuwepo na majibu yaliyokuwa yametolewa aliyasikia. Kwa msisitizo na nimejibu katika swali kutoka kwa Mheshimiwa Kigoda kwamba ni vizuri tukaweza kutumia own source kama ambavyo wao wamefanya na katika maeneo ambayo wameajiri ni pamoja na hawa wataalam wa picha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, inawezekana, kama wenzetu wa Handeni wamefanya, Liwale tunaweza. Bahati nzuri kule sasa hivi hali ya kipato inakwenda juu kabisa. Kwa hiyo, ni namna tu ya kupanga kitu gani ni kipaumbele kwa ajili ya wananchi kupata huduma. Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba kwa kupitia bajeti yake ikiruhusu tutaweza kuajiri na kupeleka watumishi wa kada ya afya.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninaomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba Zahanati ya Mangalali imefunguliwa Februari. Zahanati hii ipo katika Kata ya Ulanda na katika vijiji ambavyo bado vinaendelea kupata huduma kutoka kwenye Zahanati ya Kalenga ni Kijiji cha Makongati ambacho kutoka pale Zahanati ya Kalenga pana kilometa karibu 15, lakini pia Zahanati ya Kalenga ipo jirani kabisa na Makumbusho ya Chifu Mkwawa, lakini pia iko karibu kabisa na Barabara Kuu iendayo Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, kwa kuwa mpango wa Serikali ni kila Kata kuwa na Kituo cha Afya, je, Serikali iko tayari kuunga mkono jitihada za wananchi wa Kalenga walio tayari kutoa eneo lao na sehemu ya nguvu kazi kwa ajili ya kupatiwa Kituo cha Afya? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeelezea jinsi ambavyo hakuna uwezekano wa kuongeza majengo katika Zahanati ya Kalenga kutokana na eneo lile kwamba lina makazi na tayari yameshapimwa kiasi kwamba uwezekano wa kutoa compensation Halmashauri haina uwezo huo.
Mhesimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza niungane na Mbunge kwa kumpongeza kwa jinsi ambavyo anapigania suala la kuhakikisha wananchi wanapata afya iliyo bora, lakini pia na Mbunge wa Jimbo Mheshimiwa Mgimwa kwa jitihada zake. Kwa taarifa nilizopata ni kwamba mpaka sasa hivi ameshachangia mabati 100 na mifuko 80 ya saruji ili kuhakikisha kwamba Kituo cha Afya kinajengwa Kalenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vingi vinajengwa ili kupunguza msongamano ambao unajitokeza katika
Hospitali ya Mkoa wa Iringa kwani kutoka Kalenga kwenda Iringa ni kilometa 15 na pale kuna lami kiasi kwamba wananchi wana option ya kwenda hata kule, lakini lengo ni kuhakikisha kwamba wanapata huduma kwa urahisi zaidi.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lushoto lina Kituo cha Afya kimoja tu, lakini kwa juhudi za wananchi wamejitahidi kujenga Vituo vya Afya viwili, ambapo kituo cha kwanza kipo Ngwelo, Kituo cha pili kipo Gare. Je, nini kauli ya Serikali juu ya kumalizia vituo vile vya afya ili wananchi waweze kupata huduma wasiende mbali kufuata huduma za afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake Mheshimiwa Shekilindi anasema tayari wameshajenga Vituo vya Afya viwili, lakini kwa bahati mbaya hajafafanua vimejengwa to what extent? Kama vimekamilika au la! Maana kama vimekamilika, kinachotakiwa ni kuhakikisha kwamba huduma inapatikana kwa kupeleka Waganga pamoja na Wauguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vyote vinakamilika na viweze kutoa huduma ambayo tunakusudia na hasa upasuaji wa dharura kwa akina mama na watoto. Kwa hiyo, naamini baada ya kujua status ya hivyo Vituo vya Afya ambavyo vimejengwa kwake, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba inachangia ili huduma hiyo ambayo tumeikusudia, iweze kutolewa.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, asante na Mheshimiwa Naibu Waziri asante kwa majibu mazuri. Kwa kuwa kituo hiki kinahudumia zaidi ya Kata Tano, Kata ya Mtina, Lukumbulem Mchesi, Masakata na Tuwemacho.
Je, ni lini sasa Serikali itaona umuhimu wa kuboresha kituo hiki ili kiweze kutoa huduma za upasuaji kwa wakina mama na wajawazito?
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kampeni ya mwaka 2010 Rais wa Awamu ya Nne alitoa ahadi ya kujenga kituo cha afya katika Kata mbili za Nalase ambazo zipo katika Mji mmoja na Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imekuwa inatenga kila mwaka na mpaka sasa imeishia kujenga msingi tu. Je, ni lini Serikali itaona haja ya kutimiza ahadi ile ya Rais wa Awamu ya Nne ili wapate kituo cha afya pale Nalasi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu nimpongeze kwa dhati jinsi ambavyo Mheshimiwa Mpakate anapigania kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata huduma ya afya iliyo bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la kwanza ameuliza lini, na unaweza ukaona nia njema ya Serikali jinsi ambavyo inahakikisha huduma ya afya inapatikana na hasa katika ujenzi wa vituo vya afya katika kata husika. Hii ndio maana katika Halmashauri yake tumeanza na hiyo Kata ya kwanza na hiyo kata nyingine kwa kadri pesa itakavyopatikana. Nia njema ya Serikali ni kuhakikisha vituo vya afya vinajengwa katika kata zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, ni kweli kwamba kuna ahadi iliyotolewa na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Nne kwamba vingejengwa vituo vya afya katika kata mbili alizozitaja na yeye mwenyewe amekiri kwamba katika hizo kata mbili kazi ambayo imefanyika mpaka sasa hivi ni ujenzi wa msingi. Naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na wananchi aendelee kuwahimiza ujenzi sio msingi tu, hebu waendelee kujenga mpaka kufikia usawa wa lenta na Serikali itaenda kumalizia ujenzi huo.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Wilaya ya Karatu ina zaidi ya umri wa miaka 20 na haina hospitali ya wilaya. Hivi sasa uongozi wa wilaya unakamilisha taratibu za kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Je, Serikali iko tayari sasa kuanza kutenga fedha katika bajeti inayokuja ili kuanza ujenzi wa hospitali hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba Serikali iko tayari kuanza kutenga, nia na azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba ujenzi wa Hospitali za Wilaya unafanyika katika Wilaya 64 zote ambazo hatuna hospitali za Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ambavyo yeye mwenyewe amesema katika swali lake, ndiyo wameanza kutenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Naomba tuongeze kasi ya kutenga hilo eneo, lakini pia kutokana na Halmashauri yenyewe kwa sababu ni hitaji letu, tuanze kutenga pesa na Serikali ije kumalizia.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa kunipa nafasi hii, kwa kuwa Kituo cha Afya cha Mwese ni cha muda mrefu sana, kina zaidi ya miaka 40 hakijafanyiwa ukarabati wa aina yoyote na Serikali iliahidi kukikarabati kituo hicho. Je, Serikali ni lini itapeleka fedha kwa ajili ya kituo hicho ili kiweze kuwasaidia wananchi wa Kata hiyo ya Mwese?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya Mwese ambacho ni cha muda mrefu, je, ni lini Serikali itakuwa tayari kutenga pesa ili kufanya ukarabati?
Mheshimiwa Naibu Spika, utakubaliana kwamba ni kiu ya Waheshimiwa Wabunge wengi wangependa vituo vya afya viweze kukarabatiwa, na ndiyo maana Serikali kwa kujua umuhimu huo tumeanza na vituo vya afya 205, si haba. Naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira awamu kwa awamu na kwa kasi tunayoenda nayo naamini muda si mrefu na kituo cha afya cha kwake kitapata fedha.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, Serikali imesema kwamba itakarabati vituo 205 kikiwemo pia na Kituo cha Afya cha Malya, ninapenda kujua Mheshimiwa Waziri, ni formula gani mnayotumia kupelekwa kwa baadhi ya vituo vya afya shilingi milioni 500 na vingine milioni 400 wakati mlichagua kwamba vituo vyote 205 vikarabatiwe kwa pamoja. Ni formula gani mnayotumia? Lakini ni lini pesa zingine ambazo mliahidi kwamba mtapeleka shilingi milioni 500 kwa kila kituo, kwa nini 400 na kwa nini 500? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni formula gani ambayo inatumika katika kupeleka kupeleka fedha katika vituo vya afya sehemu nyingine milioni 500 sehemu nyingine milioni 400?
Mheshimiwa Naibu Spika, formula zipo nyingi, kwanza ya kwanza inategemea na source of funding, ni nani ambaye ameleta fedha ili ziweze kwenda kwenye kituo cha afya. Lakini pia formula nyingine ni namna ambavyo ukarabati unaohitajika, kuna baadhi ya maeneo ni majengo machache tu ndiyo ambayo yanaongezwa kiasi kwamba ikipelekwa shilingi milioni 400 inatosha kabisa kuweza kufanya ujenzi ule ukakamilika. Kwa hiyo, inategemea source lakini pia na ukarabati ni kwa kiasi gani unakwenda kufanyika katika eneo husika.
MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Ikumbukwe kuwa Mji huo wa Kibaha ndio Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani wenye Wilaya sita na yenye idadi ya watu zaidi ya 1,100,000, Mji huu wa Kibaha umekuwa unaongoza katika ujenzi wa viwanda ukiwa na viwanda vikubwa sita, vya kati 16, vidogo 78, vinavyoendelezwa kujengwa vitatu na ambavyo vipo katika taratibu za ujenzi kwenye makaratasi 20.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukipata kikwazo kikubwa hasa kwa wawekezaji hasa wanapotaka kuendeleza viwanda wanapobaini kwamba huu ni mji tu na wala hauna hadhi ya Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo basi na tukizingatia kwamba Sera Kuu ya Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwenda katika uchumi wa kati ni viwanda na inatekelezwa vizuri na kipekee na kwa kuongoza kwa mji wa kibaha, ni kwa nini sasa Serikali isitoe upendeleo wa pekee na kuupatia mji huu hadhi ya manispaa ili tuweze kwenda kwa kasi kulingana na sera ya Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wa Kibaha kwa utiifu na unyenyekevu kabisa wanaomba ombi lao hili lipewe uzito wa kipekee. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nimsifu Mheshimiwa Silvestry Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini kwa jinsi anavyopangilia hoja zake kwa niaba ya wananchi wa Kibaha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa vigezo vilivyowekwa na mwongozo wa Serikali wa mwaka 2014 bado tunahimiza kwamba Halmashauri ya Mji wa Kibaha ifanye kila linalowezekana ili kuweza kutimiza vigezo hivi nilivyovitaja mwanzoni kwenye jibu la msingi ili waweze kufikia hadhi ya kupandishwa kuwa Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi kwa kweli tunaungana nao wakazi wa Kibaha. Ni mji wa muda mrefu na sisi tunashangaa kwa nini hawajaweza kuwavutia watu wengi waongezeke kwenye Mji. Hii idadi ya watu wote waliotaja inafanana na idadi ya wakazi wa Mkoa mzima wa Pwani. Kwa mujibu wa sensa iliyofanyika mwaka 2012, Mji wenyewe wa kibaha ambao ndio uko kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha ulikuwa na wakazi 128,488, hizo ndizo taarifa tulizonazo. Kwa hiyo pamoja na kutilia uzito ombi lake bado tunahimiza kwamba Mji wa Kibaha wajitahidi kutimiza vigezo vilivyowekwa. Ahsante sana.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza. Bagamoyo imepata hadhi ya Mamlaka ya Mji Mdogo mwaka 2005 na miaka 10 baadaye mwaka 2015 baada ya kujitathimini na kuona tumetimiza vigezo tumeomba kupandishwa hadhi kuwa Halmashauri ya Mji. Je, Serikali inatupa jibu gani kuhusu Bagamoyo kupandishwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tulipokea maombi ya Mji wa Bagamoyo kupandishwa hadhi kuwa Halmashauri ya Mji sawa sawa na ambavyo tumepokea maombi mengi ya aina hiyo. Kwa sababu kupandisha hadhi Mji kuwa Halmashauri ya Mji kunaweza kusababisha ongezeko la mahitaji mengi ya kiutawala, bado maombi hayo yako kwenye mchakato na tutayafikiria muda utakapofika na kuzingatia na uwezo wa Serikali.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja. Ningependa kujua Wilaya ya Nyangh’wale Makao yake Makuu ni Karumwa, lakini nikiuliza kila mara hapa kuhusu GN ya Makao Makuu ya Wilaya Nyangh’wale ambayo ni Karumwa, leo hili swali ni mara ya tano, kila nikiuliza naambiwa GN iko tayari lakini cha ajabu mpaka leo hatujakabidhiwa katika Halmashauri yetu ya Nyangh’wale. Je, GN hiyo tutakabidhiwa lini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba uniruhusu nitoke na Mheshimiwa Amar mara baada ya kipindi hiki twende kwenye Idara yetu ya Sheria ili tuweze kumpatia majibu sahihi.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwanza naipongeza Serikali kwa jitihada zake za kuongeza pesa katika Sekta ya Afya na kuwezesha ujenzi huu na upanuzi wa vituo viwili hivi vya Iboya na Masumbwe. Je, Serikali sasa itakuwa tayari kuruhusu bajeti ya mwaka huu ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mbogwe uanze baada ya mwaka huu kuiondoa hiyo bajeti kutokana na ukomo wa bajeti kwa maana ya ceiling. Ceiling ili-burst kwa hiyo, ile hela ambayo tulikuwa tumepanga kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya iliondolewa. Je, Mwaka huu wa Fedha itaruhusiwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, yamekuwepo madai ya muda mrefu ya watumishi ya uhamisho kutoka katika Wilaya mama ya Bukombe kuja Wilaya ya Mbogwe wakiwemo Watumishi wa Idara ya Afya hawajalipwa. Je, malipo haya yatafanyika lini ili kuondoa usumbufu kwa watumishi hawa ambao wamekuwa wakidai kwa muda mrefu. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa niaba ya Serikali tunazipokea pongezi zake za dhati maana yeye mwenyewe anakiri kwamba vituo viwili kwanza kujengwa kwa milioni 400, jumla milioni 800 siyo haba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anataka kujua je, Serikali itaruhusu ujenzi wa Hospitali ya Wilaya baada ya kwamba haikuwezekana kutokana na ufinyu wa bajeti. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote Wilaya zote 64 na jana nilijibu, ambazo hatuna Hospitali za Wilaya, hospitali zinajengwa. Ninachoomba kwa kupitia Halmashauri yake ni vizuri wakatenga eneo na wao wakaanza ujenzi ili Serikali ije kukamilisha ujenzi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili anauliza kuhusiana na suala la kuwalipa Watumishi ambao walihamishwa kutoka maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wilayani kwake, lini watalipwa. Mara baada ya uhakiki kukamilika na Mheshimiwa Rais alilisema, kati ya madeni ambayo yanatakiwa kulipwa ni pamoja na madeni ya Walimu pamoja na Watumishi wa Afya. Zoezi hili litakamilika muda si mrefu.
MHE. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote niwashukuru wananchi wa Songea Mjini kwa kunichagua kuwa Mbunge na kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu. Pili nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi, Chama Tawala. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatizo lililopo katika Jimbo la Mbogwe ni sawa na tatizo ambalo lipo katika Jimbo la Songea Mjini katika ujenzi wa Vituo vya Afya hususan katika Kata tatu za Ndilimalitembo, Ruvuma na Likuyufusi ambazo wananchi wamejitolea kwa mguvu na wanahitaji msaada wa Serikali. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya katika Kata ya Ndilimalitembo, Kata ya Ruvuma na Kata ya Likuyufusi? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kumpongeza kwa ushindi wake na karibu sana Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake anataka kujua lini Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kukamilisha vituo vya afya katika Kata zake hizo mbili. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vya afya vinajengwa tena vinajengwa vingi ili kuondoa adha ya matibabu kwa wananchi kwa kutokwenda umbali mrefu kupata huduma ya matibabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanza na vituo 205 baada ya hivi 205 kukamilika ni azma ya Serikali kuhakikisha na maeneo mengine na hasa ambayo kuna upungufu mkubwa na hasa kwa mijini kumekuwa na msongamano mkubwa sana wa wananchi kufuata huduma ya afya katika hospitali za Mikoa na Wilaya. Ni azma yetu kuhakikisha kwamba vituo vya afya vinajengwa ili kupunguza mrundikano ikiwa ni pamoja na maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. EZEKIEL G. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza:
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Msalala kama ambavyo umesikia maeneo mengine haya mawili ambayo yameuliziwa maswali Songea Mjini na Mbogwe, wao pia wana maboma ya zahanati na vituo vya afya na bahati nzuri wenyewe wamekwenda mbali zaidi, kuna maeneo ambapo kumetajwa kwamba maboma yako kwenye lenta. Wananchi wa Jimbo la Msalala wana vituo vya afya vinne ambavyo vimekwishakamilika maboma yake, zahanati 38 ambazo zimekwishakamilika maboma yake. Maboma haya yamejengwa zaidi ya miaka mitatu na sehemu vimeanza kubomoka. Imefika mahali sasa wananchi wanagomea michango mingine wakisema kamilisheni kwanza miradi tuliyokwishaianza.
Nataka tu kujua toka Serikalini ni lini sasa Serikali na yenyewe italeta nguvu yake ambayo wastani ni kama bilioni ili kukamilisha maboma haya 42, manne ya vituo vya afya na 38 ya zahanati, Msalala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa dhati kabisa nianze kwa kumpongeza kwa jitihada kubwa ambazo anafanya kwa wananchi wa Jimbo la Msalala, kwa ujenzi mkubwa ambao umefanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiongea mara nyingi alichokuwa anaomba kwanza katika hizi pesa ambazo zimepatikana zikitumika zikakamilisha hayo majengo ambayo yanatakiwa kujengwa katika vituo vya afya, anataka hicho kiasi kinachobaki kipelekwe kwenye maeneo mengine. Jambo ambalo Serikalini wala hatuna ubishi nalo ni kuhakikisha kwamba jitihada za wananchi na tukibana vizuri pesa zikatumika maeneo mengine yaweze kujengwa kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa vituo vya kutolea afya 1,845 na hivi tutavikamilisha.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza; Serikali ina mpango gani wa kuajiri watumishi wa sekta ya ardhi ikiwemo Kibiti ambako kuna watumishi wachache?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia vifaa vya upimaji katika Wilaya mpya ya Kibiti kwa sababu mapato yake ya ndani yamekuwa madogo sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uchache wa watumishi wa ardhi, naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge na ninaamini kabisa ana nia njema na amekuwa akipigania wananchi wa jimbo lake; katika ikama ambayo itakuwa imewekwa na halmashauri yake ni vizuri wakaonesha uhitaji wake na halafu utaratibu wa kuwaajiri watumishi wa ardhi kama ambavyo ilikuwa kwa watumishi wengine ikafuatwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, uwezo wa Halmashauri ni mdogo kwa hiyo wanaomba vifaa vya kupimia ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi ambayo ndiyo Wizara yenye dhamana kwa kujua iko haja kubwa ya kuhakikisha kwamba ardhi inapimwa katika maeneo yote na Wilaya zote, juzi juzi Serikali kwa kupitia Wizara ya Ardhi wameweka katika mpango wa kuhakikisha kwamba Wilaya zote zinanunuliwa vipima ardhi ili iweze kurahisisha suala hili. Naamini na wao watakuwa wanufaika.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza, lakini kabla ya kuuliza maswali haya, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais na Serikali kwa utaratibu uliowekwa sasa wa kuhakikisha hakuna mwalimu anahama mpaka stahiki zake zinalipwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu mawili ni kama ifuatavyo; naishukuru Serikali imeongeza annual increment kwa walimu lakini ni lini Serikali itawapandishia mishahara? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa nini walimu wanachukua muda mrefu kupandishwa madaraja? Kuna walimu tangu mwaka 2012 mapaka hivi sasa walitakiwa wawe wamepandishwa zaidi ya mara tatu lakini mpaka sasa walimu hawa hawajapandishwa daraja hata mara moja. Je, ni nini majibu ya Serikali? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Innocent Bashungwa kwa kazi anazozifanya ikiwemo ushauri wa mara kwa mara anaoutoa kwa Serikali na sisi tunaupokea na pongezi alizotoa kwa Mheshimiwa Rais, tutamfikishia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameshukuru kuhusu annual increment, sasa ameuliza ni lini Serikali itapandisha mishahara. Utaratibu huu ambao ulikuwa umesimama kwa kipindi kifupi cha miaka kama miwili hivi kupisha uhakiki wa watumishi, zoezi ambalo limefanywa kwa umahiri na weledi mkubwa, baada ya kuwa tumelikamilisha sasa tutaingia kwenye awamu ambayo tutaboresha maslahi ya watumishi ikiwemo mishahara yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu walimu ambao hawajapandishwa daraja kwa muda mrefu. Mimi napenda nikiri kwamba Serikali haijapandisha daraja kuanzia kipindi cha mwaka 2016 hadi 2017, lakini kuanzia mwaka huu wa fedha, matayarisho yanaendelea huko mengi kwa ajili ya kuwapandisha madaraja ikiwemo kuwapandisha wale ambao walistahili kupandishwa tarehe 01 Julai, 2016 na wale ambao walistahili kupandishwa moja mwezi wa saba mwaka 2017 watapandishwa kwa pamoja kwa mserereko. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Pamoja na changamoto nyingi zilizokuwa zinakabiri kundi hili la walimu, moja ya changamoto kubwa inayokabili kundi la walimu ni mazingira magumu ya kufanyia kazi. Na kwa kuwa hivi sasa Serikali yetu inatekeleza mpango kabambe wa vituo vya afya kwa nchi nzima, je ni kwa nini Serikali isione umuhimu sasa wa kushirikiana na jamii, Halmashauri na Serikali Kuu ili kuona ni namna gani kwa kila Halmashauri katika mwaka wa fedha tunajenga nyumba kadhaa za walimu hasa mazingira yale ya vijijini ili walimu waweze kufanya kazi zao katika mazingira mazuri. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Zacharia Issaay kwa swali lake zuri na ninaomba sasa kumjibu kwamba Serikali inakubaliana kwamba kuna maeneo ambayo kweli yana mazingira magumu hasa maeneo ambayo yapo mbali na Makao Makuu ya Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo hayo yanahitaji mkakati maalum, na kama tulivyoeleza katika mipango mingi ya Serikali, ni kwamba tunaomba sana ushiriki wa jamii katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na miundombinu ambayo inavutia walimu waendelee kukaa katika maeneo hayo na miundombinu hiyo ni pamoja na nyumba za walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili natoa wito kwamba halmashauri zote ziweke kipaumbele kwenye maeneo ambayo yapo mbali zaidi na halmashauri kwa kutenga kwanza fedha/mapato ya ndani kabla hatujapeleka sisi kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya kukamilisha maboma. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikuliza swali hili toka nilivyoingia ndani ya ukumbi huu mwaka 2010. Ujenzi wa hospitali hii umeanza toka mwaka 2007 mpaka hivi tunavyoongea fedha inayoonekana hapo ndiyo ambayo imeshafika katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, lakini wakati nauliza maswali yangu mawili ya nyongeza, nipongeze Serikali kwa hatua kubwa ambayo wameamua kuchukua katika uboreshaji wa vituo vya afya kikiwemo Kituo cha Afya cha Tinde. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, je, Serikali inawaahidi nini wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kuhusu ukamilishwaji wa ujenzi huu kwa kuwa umekuwa ni wa muda mrefu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali imeweka mpango gani madhubuti ili kuhakikisha kwamba pindi ujenzi huu wa vituo vya afya unapokuwa umekamilika unaweza kupata wataalam wa kutosha katika majengo yetu ya upasuaji na huduma zingine zinazostahili? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika na mimi tangu nimemfahamu Mheshimiwa Azza amekuwa akipigania ujenzi wa hospitali, lakini kama hiyo haitoshi ni pamoja na kupigania Vituo vya Afya na Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga. Naomba kwa pekee nimpongeze kwa jitihada zake hizo na ndizo ambazo zimezaa upatikanaji wa vituo vya afya viwili, kwa maana ya Kituo cha Afya Tinde na Kituo cha Afya Samuye ambacho kimoja ni shilingi milioni 400 na kingine milioni 500.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukija upande wa maswali yake, anataka ahadi ya ukamilishaji wa hospitali hizo. Kama ambavyo nimekuwa nikijibu hapa, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa hospitali 64 katika Wilaya ambazo hazina Hospitali za Wilaya na hasa kwa wananchi wa wilaya yake ambao wameshaonesha moyo kwanza kwa kutenga eneo lakini pia ujenzi umeshaanza na ndio maana OPD imeweza kukamilika. Kwa kadri bajeti itakavyoruhusu hakika naomba nimuhakikishie tutatupia jicho letu kuhakikisha kwamba hospitali hiyo inakamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ametaka kujua juu ya suala zima la hospitali inapokamilika na wataalam wawepo. Naomba nimuhakikishie, ni azma ya Serikali, si suala la kujenga majengo tu, tunataka tujenge majengo ambayo yatumike. Kwa hiyo, pale ambapo ujenzi unakamilika na wataalam watakuwa wamepatikana ili waweze kutoa huduma kwa wananchi waliokusudiwa. (Makofi)
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Tarime tumejitahidi na Mheshimiwa Kandege alikuwepo, tumejenga hospitali kubwa pale ya Wilaya ambayo iko Nyamwaga, tumejenga vituo vya afya karibia vine, kuanzia Nyandugu, Mriba na Sirari ambako ni kituo ambacho Waziri Mkuu alisema kiwe cha mfano nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa shida yetu ni watumishi, ni lini mnatuletea watumishi hasa kwenye Hospitali ya Nyamwaga ambayo tumeshanunua na vifaa ili ile hospitali ianze kuhudumia wananchi wa Tarime ambao wamefanya kazi kubwa pale kuijenga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maneno kwamba wakifanya vizuri upande wa Upinzani hatuwapongezi, lakini kwa dhati kabisa naomba nipongeze kazi nzuri ambayo imefanywa na wananchi wa Tarime akiwepo na Mbunge Mheshimiwa Heche kwa sababu tumeenda tukatizama kwa macho na kuona ni kusadiki, mmefanya kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Heche atakubaliana na mimi kwamba katika ziara aliyofanya Mheshimiwa Waziri Mkuu, aliahidi kwamba taratibu zikamilike mara moja ili Hospitali ya Nyamwaga ianze kufanya kazi na tena ni matarajio yetu kwamba muda sio mrefu itakuwa ni miongoni mwa Hospitali za Wilaya. (Makofi)
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, na pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana kaka yangu, Mheshimiwa Selemani Jafo na Dada Jenista Mhagama. Baada ya kufika Karagwe na kukuta wilaya ambayo ina watu takribani 360,000 ina Kituo cha Afya kimoja cha Serikali waliweka nguvu na Serikali sasa imetusaidia tumekamilisha hicho Kituo cha Afya cha Kayanga, nawashukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza; swali la kwanza, kwa vile Wilaya ya Karagwe ina Kituo cha Afya kimoja cha Serikali, na hivi sasa naishukuru TAMISEMI tunaenda kukamilisha Kituo cha Afya cha Nyakayanja, mnaonaje wakati mchakato wa kujenga Hospitali ya Wilaya unaendelea mtupe angalau vituo vya afya viwili ili ku-balance jiografia ya Karagwe?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa TAMISEMI na Wizara ya Afya wanafanya kazi nzuri, mnaonaje mkae na development partners kwa sababu Kamati ya Huduma za Jamii inaonesha kwamba kuna Wilaya 67 katika nchi yetu ambazo bado hazina Hospitali za Wilaya. Sasa kwa sababu Serikali inafanya kazi nzuri ya kutoa huduma mnaonaje mkae na development partners ili mtengeneze proposal ambayo itatusaidia kukamilisha ujenzi wa Hospitali 67 za Wilaya? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumpongeza ndugu yangu, Mheshimiwa Bashungwa kwa jinsi ambavyo anapigana katika jimbo lake kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata huduma ya afya iliyo bora. Katika maelezo yake anaongelea kwamba kuna kituo cha afya kimoja, ni kiu yake kwamba vituo vya afya vingeongezeka walau viwili tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vya afya vinajengwa katika maeneo yote na kwa kufuata uwiano sawia. Kwa hiyo, katika awamu inayokuja naomba nimhakikishie kwamba walau tutahakikisha kwamba kituo kingine cha afya kinapelekwa kule haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anauliza uwezekano wa Serikali kushirikiana na development partners katika kuhakikisha kwamba tunaenda kumaliza tatizo la ujenzi wa Hospitali za Wilaya. Ni nia ya Serikali na milango iko wazi kwa yeyote yule ambaye ana nia njema ya kusaidia Serikali katika ujenzi wa Hospitali za Wilaya, tunamkaribisha, ilimradi katika yale masharti ambayo yatakuwa si ya kudhalilisha nchi yetu, sisi kama Serikali tuko tayari.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mkoa wa Tabora Wilaya mbili hazina Hospitali za Wilaya, Sikonge na Tabora Manispaa na viwanja tayari vipo, je, Serikali inasema nini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la la Mheshimiwa Mwanne Mchemba, ambaye wakati tumefanya ziara kwenda Kilolo yeye ndio alikuwa Mwenyekiti wa Kamati na akashuhudia kazi njema ambayo inafanywa na Serikali, Hospitali ya Wilaya ya Kilolo itakuwa miongoni mwa hospitali za kutilia mfano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika swali lake anasema Serikali inasema nini kuhusiana na Wilaya mbili za Sikonge na Tabora Mjini ambazo hazina Hospitali za Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu katika majibu yangu ya mwanzo, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo hakuna hospitali za wilaya zinajengwa ili kupunguza mlundikano wa wagonjwa kwenda katika Hospitali za Rufaa ili wale ambao wanaweza kutibiwa katika Hospitali za Wilaya waweze kutibiwa. Naomba niiombe Halmashauri, ni vizuri na wao wakaonesha kwamba ni hitaji la wananchi kwa hiyo na wao katika vyanzo vyao vya mapato waanze pia ujenzi ili na Serikali Kuu tuweze kushirikiana nao.
MHE. LIVINGSONE J. LUSINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Naibu Waziri kwa majibu, hata hivyo napenda kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; urefu wa barabara alizotaja na milioni 350 kweli hapo kuna matengenezo ya barabara kwa kiwango cha changarawe au ni kwa kiwango cha tope?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mvua za mwaka huu Mungu ametupa neema zimekuwa nyingi na zimetusaidia sana kwa upande wa kilimo, vilevile zimeleta uharibifu mkubwa sana wa barabara na madaraja, Mheshimiwa Waziri anatuambiaje juu ya matengenezo mazuri na yenye maana kwa ajili ya wananchi kuweza kupitisha mazao yao ambayo wanategemea kuyavuna ili waweze kujiletea maendeleo? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, anaulizia juu ya idadi ya kilometa ambazo nimezitaja na kiasi cha fedha ambacho kimetumika je, tumetengeneza kwa ubora uliotarajiwa au tumeyatengeneza kwa kutumia tope.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza hatujatumia tope kwa sababu yeye mwenyewe ni shuhuda kwamba tumehama kutoka katika matengenezo yaliyokuwa yanafanywa na Halmashauri pale ambapo kila Mheshimiwa Diwani alikuwa akiomba angalau apate hata kilometa moja au kalivati moja katika aeneo lake, mwisho wake inakuja inafikia kwamba hata ile thamani ya pesa ambayo imetumika haikuweza kuonekana na hivyo tukawa tunarudia kila mwaka katika matengenezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Lusinde na bahati nzuri na yeye ni shuhuda amekuwa akifanya kazi nzuri ya kupita kwenye Jimbo lake hebu akalinganishe kazi ambayo imefanywa na chombo hiki cha TARURA linganishe na jinsi ambavyo kazi zilikuwa zinafanyika hapo awali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili ameongelea neema ya mvua ambayo tumepata na sisi sote tukiwa ndani ya Mkoa wa Dodoma ni mashuhuda, tumepata mvua ya kutosha, mvua ni neema, lakini kila neema nayo inakuja na dhahama yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, naomba nimhakikishie chini ya TARURA na ndiyo maana kuna maeneo ambayo kumekuwa na mataengenezo na maombi maalum ili kuhakikisha kwamba barabara hizi zinapitika vipindi vyote na kiasi cha pesa ambacho chombo hiki kimeombewa kama Bunge lako Tukufu itaidhinisha chini ya usimamizi madhubuti hakika barabara zitatengenezwa kwa kiwango kizuri na kitakachoweza kupita katika vipindi vyote.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ninachotaka kujua TARURA ni chombo ambaco kimeundwa hivi karibuni, nataka kujua TARURA sasa kwa sababu barabara wanazoshughulikia ni zile zilikuwa zinashughulikiwa na Halmashauri chini ya Madiwani. Je, hiki chombo sasa kinasimamiwa na mamlaka gani kwa niaba ya wananchi, kwa sababu hawaingii kwenye Baraza la Madiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba TARURA ni chombo ambacho kimeanzishwa hivi karibuni. Kimsingi taarifa ya kazi zinazofanyika taarifa yake inapelekwa kwenye chombo kinaitwa DCC na katika DCC Waheshimiwa Wabunge wote wanakuwemo kwenye kile chombo, lakini pia kila Mwenyekiti wa Halmashauri husika anahudhuria kwenye hicho kikao na ndiyo fursa ambayo kwa sasa hivi TARURA inatoa taarifa juu ya utekelezaji wa kazi zake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, hata katika vipaumbele vya barabara ambazo zinaenda kutengenezwa ni wajibu wa Halmashauri kwa kushirikiana na Madiwani wote tunaidhinisha barabara ambazo ni vipaumbele, lakini TARURA inapelekewa kulingana na bajeti sasa wao ndio wanasema katika hizi barabara tunaenda kutengeneza barabara zipi, lakini fursa kama forum ya Waheshimiwa Madiwani bado ipo.
MHE. ABDALLAH S. MTULIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Alhamdulilah. Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana, lakini pia nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima, nina afya njema, akili timamu na utayari wa hali ya juu ya kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Kinondoni na tunasema dua la mwewe halimpati kuku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo letu la Kinondoni na Manispaa ya Kinondoni kwa ujumla TARURA inafanya kazi vizuri, tunawapongeza sana. Hata hivyo, Manispaa yetu ya Kinondoni ina barabara za kiwango cha lami siyo zaidi ya asilimia 10 za barabara zote katika Manispaa ya Kinondoni na tumewaambiwa wananchi tunataka kuleta Kinondoni mpya; je, TARURA ina mpango gani wa kutuongezea barabara zetu katika kiwango cha lami ili angalau kufikia asilimia 50 kama siyo asilimia mia moja?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI) - MHE. JOSEPH S. KANDEGE:
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa, welcome again uko katika nafasi iliyo sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo chombo chetu TARURA kinafanya kazi vizuri ni pamoja na Manispaa ya Kinondoni, nimepata fursa ya kwenda kutembelea, Halmashauri zingine zinatakiwa kwenda kuiga na kutazama kazi nzuri ambayo inafanywa na TARURA Kinondoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la kuongeza ili angalau tufike asilimia 50 ya barabara zote kuwa za lami, kati ya Miji ambayo ina fursa ya kupata maendeleo kwa maana ya miundombinu ya barabara ni pamoja ni Jiji letu la Dar es Salaam. Naamini katika mpango mzima wa kuboresha Jiji la Dar es Salaam na program zinazoendelea hakika, barabara za Kinondoni zitahama kutoka hiyo asilimia kufika asilimia 50 katika kipindi ambacho siyo kirefu sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI): Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu niongezee katika majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba katika eneo la Kinondoni ambako Mbunge aliyeapishwa leo Mheshimiwa Mtulia anatoka ni kwamba hiyo coverage tutaifika haraka sana kwa sababu tuna combination mbili; tuna mradi wa DMDP ambao Mheshimiwa Mbunge anaufahamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu una kazi kubwa sana ya kuboresha miundombinu ya barabara za lami katika Jiji la Dar es Salaam na eneo la Kinondoni ni eneo moja wapo, lakini kuna upande mwingine upande wa TARURA, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aondoe hofu zile ahadi alizozisema kwa wananchi wake, naamini ikifika mwaka 2020 zote zitakuwa zimetekelezwa tena kwa zaidi.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Hata hivyo, nitumie fursa hii kuwashukuru wananchi wa Siha kwa kuniamini tena na kuhakikisha hawa wanaosema muda nawapiga kipigo ambacho hawajawahi kukisikia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna barabara yetu ya kutokea Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kwenda kwenye Kata ya Biriri kukutana na barabara inayotokea Sanya Juu kuelekea mpaka KIA (Kilimanjaro International Airport), kwa mwaka jana ni katika barabara mbili ambazo zilikuwa zipandishwe hadhi kuingizwa TANROAD ikashindikana ikawa imepanda barabara moja ya Mwanga. Nataka kumuuliza Waziri mwaka huu basi isidunde kama zawadi ya watu wa Siha kwa uamuzi wa busara walioufanya. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI) - MHE. JOSEPH S. KANDEGE:
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze na kumkaribisha sana Dkt. Mollel na kumhakikishia kwamba yuko katika nafasi ambayo ni salama sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kupandisha hadhi barabara ambayo anaiongelea ili iwe chini ya TANROAD.
Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni shuhuda kwamba Waheshimiwa Wabunge wengi tulikuwa tunapenda barabara za Majimboni kwetu zipandishwe zichukuliwe na TANROADS, lakini ni kwa nini tulikuwa tunataka zichukuliwe na TANROADS? Ni kutokana na namna ambavyo barabara ambazo ziko chini ya TANROADS zimekuwa zikihudumiwa kwa namna nzuri. Ndiyo maana kama Bunge tukaona kwamba ni vizuri tukaanzisha chombo ambacho kitakuwa kinafanya kazi madhubuti kama ambavyo zimekuwa zikifanywa na TANROADS.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie, kwa kasi ambayo tumeanza nayo na jinsi ambavyo TARURA imeanza kufanya kazi, nimtoe mashaka, barabara ambayo anaisemea chini ya TARURA itakuwa na hadhi na ubora sawa na barabara ambazo zinatengenezwa chini ya TANROADS.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mvua zinazoendelea zimeharibu barabara nyingi sana za vijijini karibu nchi nzima mfano katika Jimbo langu la Rombo barabara nyingi sana za vijijini hazipitiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua TARURA inafanya kazi nzuri sana sasa hivi katika baadhi ya majimbo. Natambua pia kwamba kuna bajeti itasomwa hapa kwa ajili ya kuiwezesha TARURA kuendelea na kazi zake. Je, Serikali ina mpango wowote wa dharura wa kuisaidia TARURA ili iweze kuwezesha barabara ambazo zimevunjika vijijini kupitika kwa sasa hivi ili wananchi waweze kupeleka mazao yao katika masoko na kadhalika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mvua zimenyesha kubwa katika maeneo mengi na kila neema inavyokuja huwa inakuwa na adha yake. Ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba barabara zote zinapitika kwa vipindi vyote. Ni vizuri tukapata fursa ya kufanya uthamini maeneo ambao yameharibiwa na mvua ili hatua za dharura ziweze kuchukuliwa na wananchi wetu wasiweze kuendelea kupata shida.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niulize swali dogo la nyongeza. Kuna ahadi nyingi tuliwaahidi wananchi wetu wakati tukiomba kura ikiwemo Mheshimiwa Rais kuahidi wananchi wa Itigi kuwajengea barabara ya lami inayoingia katika Mji wa Itigi kilometa nane. Je, ni lini sasa Wizara hii itatekeleza ahadi hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna ahadi nyingi ambazo zilitolewa wakati wa kampeni na yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge alitoa ahadi zake na Mheshimiwa Rais alitoa ahadi katika maeneo ambayo alienda kuomba kura. Katika kipindi ambacho aliomba na kutoa ahari ahadi utekelezaji wake ni ndani ya miaka mitano. Upo utaratibu ambao umewekwa mahsusi ili kuhakikisha kwamba ahadi zote ambazo zilitolewa na Mheshimiwa Rais zitaenda kutekelezwa. Naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, Ilani ya CCM inatekelezwa ndani ya miaka mitano na sisi ni waungwana tukiahidi huwa tunatekeleza.
MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Bado sijaridhishwa na majibu hayo ya Mheshimiwa Waziri. Kutokana na sintofahamu ya wananchi hao wa Bunda, naomba Mheshimiwa Naibu Waziri, nina evidence hapa nisome. Kutokana na kituo hicho cha afya kwa mwaka 2006, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye ni Rais Mstaafu aliweka jiwe la msingi. Aliweka jiwe la msingi ili kusudi huo upembuzi yakinifu na hivyo vitu vingine vikikamilika ipewe hati ya kuwa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kufanya huo upembuzi yakinifu anaousema hapa Mheshimiwa Waziri, mochwari imeshatengenezwa tayari na ipo, chumba cha dharura Mheshimiwa Waziri kipo, X-Ray tayari ipo, Ultra Sound tayari ipo na barua hii nitamkabidhi nikitoka hapa Mheshimiwa Naibu Waziri, ya Wilaya ile lakini pia chumba cha dhararu kipo. Je, ni nini sasa kinachosababisha hii Wilaya ya Bunda na hicho Kituo cha Manyamanyama kisipewe hadhi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa usimamizi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Bunda, Bibi Janet Mayanja akiwa na Madiwani wake chini ya Mwenyekiti wa Halmashauri kutokana na mapato na makusanyo ya Halmashauri wameweza kuweka vitu hivyo na vinginevyo. Ni kwa nini sasa hospitali hiyo isipewe hati? Kama mnatuelezea kwamba vituo vya afya vinatakiwa vibaki palepale ziwepo Hospitali za Wilaya, Mheshimiwa Waziri naomba majibu leo kwamba kama fedha ipo… (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali bado halijakwisha, naomba Mheshimiwa Waziri niambiwe kwamba ni lini sasa na sisi mtatuletea hiyo pesa ya kujenga Hospitali ya Wilaya ili tujue kile ni kituo cha afya? Mheshimiwa Naibu Waziri, tafadhali naomba majibu ya kutosha. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli idadi ya wagonjwa wanaokwenda kupata huduma katika Kituo cha Afya cha Manyamanyama ni wengi sana na ndiyo maana kumekuwa na concern ya kwamba ni vizuri kituo cha afya kile kikapandishwa hadhi ya kutoka kituo cha afya kikawa hospitali ya wilaya. Hata hivyo, ni ukweli usiopingika kwamba uhitaji wa vituo vya afya bado uko pale pale na ujenzi wa hospitali za wilaya bado uko pale pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba Mheshimiwa Mbunge pamoja na kazi nzuri ambayo anaifanya ya kuhakikisha afya za watu wake zinaimarika, ni vizuri tukahakikisha tunaheshimu ramani inayohusu hospitali ya wilaya ambayo ni tofauti na ramani inayohusu kituo cha afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hospitali za wilaya ambazo tunakwenda kuzijenga kwa mwaka wa 2018/2019, Bunda DC ni miongoni mwa Wilaya ambazo zinakwenda kupata hospitali za wilaya. Kwa taarifa nilizonazo Bunda DC na Bunda Mji, Bunda DC mpaka sasa hivi bado hawajajua wapi Halmashauri yao itakuwa. Kwa hiyo, pesa hiyo ambayo itakuwa ipo tayari kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya busara itumike ili pale ambapo papo tayari tuanze kujenga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilipata fursa ya kuongea na Mkurugenzi jana, pamoja na Kituo cha Afya cha Manyamanyama tayari Halmashauri imeanza kutafuta eneo lingine la ukubwa wa hekari 40. Kwa hiyo, thinking yao ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na eneo mbadala kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Katika Bunge lililopita niliuliza swali kuhusiana na hospitali ya wilaya ambayo tulikuwa tumeambiwa kwamba itajengwa katika Kata ya Chipaka kwenye Kijiji cha Chipaka. Sasa hivi inaonesha kwamba kuna mabadiliko ambayo yanataka kufanyika hospitali ile ikajengwe maeneo mengine ambayo hayana majengo kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo tulilokuwa tumeliteua ni eneo ambalo lilikuwa na majengo ambayo yalikuwa yanatumika kwa ajili ya mradi wa kujenga barabara kutoka Tunduma kwenda Sumbawanga, kuna majengo zaidi ya 20, leo hii wanataka kupeleka maeneo ambayo hayana majengo kabisa. Mheshimiwa Waziri aliniambia hapa atahakikisha kwamba analifuatilia jambo hili na hospitali inajengwa eneo ambalo walikuwa wametuambia kwamba ni lazima itajengwa pale. Je, amefuatilia na anatoa majibu gani kwa wananchi wa Tunduma ili wawe na uhakika wa hospitali katika eneo la Chipaka na Kata ya Chipaka? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la nyongeza la Mheshimiwa Marwa nimeeleza kwamba ramani kwa ajili ya hospitali za wilaya ambazo zimekuwa designed na Ofisi ya Rais, TAMISEMI zinajitosheleza. Katika pesa ambazo tunakwenda kuanzia tunakwenda kuanza na jumla ya shilingi bilioni 1.5 kwa ramani ambayo ni sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa asingependa tukaenda kwenye majengo ambayo hayakidhi ramani ambazo tunazo, ni vizuri tukapeana nafasi na naamini na yeye mwenyewe akiona ramani pendekezwa ataafiki kwamba ni vizuri majengo yale yakatafutiwa kazi nyingine, lakini sisi tungependa tujenge hospitali ya wilaya yenye hadhi ya kulingana na Mheshimiwa Mbunge ambaye anatoka Tunduma.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Bunge lililopita nilisimama hapa nikauliza juu ya support ya Serikali katika ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kasu, nikajibiwa kwamba siyo muda mrefu pesa zitapelekwa zaidi ya shilingi milioni 500. Nataka kujua, ni lini Serikali sasa itapeleka pesa hizo maana nimetoka Jimboni bado hatujazipokea pesa hizo? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ahadi ya Serikali kupeleka pesa kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kasu ni mara pesa itakapopatikana kwa sababu ni ahadi ambayo tumeiweka na tuko very firm katika hilo. Tutahakikisha katika mgao wa awamu inayofuata na kituo chake cha afya kinapata mgao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hiyo haitoshi, katika wilaya ambazo zinaenda kujengewa hospitali za wilaya ni pamoja na wilaya yake. Kwa hiyo, naamini adha ambayo wananchi wa Nkasi wamekuwa wakiipata kuhusiana na suala zima la matibabu litapungua muda siyo mrefu sana.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na jibu la msingi la Mheshimiwa Waziri bado kuna shida katika ujenzi unaoendelea pale Ipinda, nilikuwa nataka kujua Serikali imefuatilia gharama ya pesa ilizotoa na uhalisia wa majengo yanayojengwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ujenzi wa zahanati ni kitu kingine, lakini utendaji wa wafanyakazi ikiwemo madaktari ni shida hasa Zahanati ya Ikuti Rungwe na hapo Ipinda hakuna watendaji wa kazi. Ni lini Serikali itatoa wafanyakazi ikiwemo madaktari na hasa Madaktari Bingwa wa wanawake kusaidia wanawake wa Wilaya ya zahanati ya Ipinda lakini pia Zahanati ya Ikuti Wilaya ya Rungwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwakagenda kama ifuatavyo:-
Katika swali lake la kwanza anauliza iwapo Serikali imefuatalia kujua gharama iliyotumika na majengo ambayo yamejengwa. Majengo ambayo yanajengwa ni kwa mujibu wa ramani ambayo imetolewa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI na ni na suala ambalo matarajio yangu makubwa na Mheshimiwa Mbunge akiwa ni sehemu ya wananchi wa Halmashauri ile ni vizuri akatuambia ni sehemu ipi ambayo anadhani kwamba haridhiki, lakini mpaka sasa hivi ninavyoongea hata Mbunge wa Jimbo hajaleta malalamiko yoyote kwamba labda kuna ubadhilifu katika ujenzi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaongelea juu ya suala zima la upatikanaji wa wataalam, suala la kujenga majengo jambo moja na suala la wataalam jambo la pili, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni nia ya Serikali kuhakikisha pale tunapomaliza ujenzi na wataalam wapatikane kwa mujibu wa Ikama na jinsi mahitaji yanavyopatikana.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwanza sina budi kushukuru vyombo vya ulinzi na usalama hasa Kibiti tunalala usingizi.
Swali langu la nyongeza Kituo cha afya kibiti hasa kinazidiwa kutoa huduma, je, Serikali ina mpango gani wa kuijengea Kibiti Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli huko uhitaji mkubwa sana na kituo cha afya kilichopo kimezidiwa, naomba nimuondoe mashaka Mheshimiwa Mbunge na nimuhakikishie miongoni mwa hospitali 67 zinazotarajiwa kujengwa ni pamoja na Wilaya yake, kwa hiyo, wakae mkao wa kula Serikali inatekeleza ili kuondoa shida kwa wananchi. (Makofi)
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu nilipata ahadi kutoka Wizara hii kwamba kutapelekwa hela za ujenzi kituo kile cha Mchombe katika Jimbo la Mlimba kiliwekwa katika mpango wa Serikali na kilipata zile grade ambazo zinafaa kupewa pesa ili kuboresha Kituo cha Afya cha Mchombe ambapo kinahutubia kata zisizopungua 10. Je, na katika mpango uliopita hakuna hela iliyopelekwa, mimi tu mfuko wa jimbo nilipeleka hela kidogo kwa ajili ya kusaidia…
Je, ni lini sasa Wizara ya afya itapeleka pesa za kuimarisha Kituo cha Afya cha Mchombe ndani ya Jimbo la Mlimba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Susan Kiwanga swali lake la nyongeza juu ya ahadi ambayo anasema ilitolewa, sina uhakika juu ya ahadi hiyo, lakini kama ahadi hiyo imetolewa kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba nimuhakikishie hivi karibuni ni kama nilivyojibu swali la nyongeza jana la Mheshimiwa Mipata kuhusiana na kituo chake cha afya Kasu kuna matarajio ndani ya mwezi huu kuna pesa ambazo zitapatikana kwa ajili ya vituo vya afya visivyopungua 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sina uhakika kama katika hivyo 25 na yeye ni miongoni mwa hivyo ambavyo vinaenda kupelekewa pesa.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza kwa kuwa wanawake wengi wamehamasika sana kuanzisha VICOBA na wengine wameanzisha vikundi mbalimbali kwa lengo la kujikwamua kimaisha lakini wamekuwa wakiangaishwa sana kwa kupata hiyo asilimia 10; sasa ni lini Serikali itaweka mazingira mazuri ili hata kama hiyo asilimia 10 ipo lakini wawekewe mazingira mazuri ya kupata mikopo kwenye mabenki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa kuwa asilimia 10 ya wanawake, walemavu na vijana inachelewa sana kuwafikia walengwa; sasa basi kwa nini Serikali isipunguze masharti ya kukopa kwenye mabenki ili wanawake waweze kukopa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba ukilinganisha masharti yaliyopo katika upatikanaji wa hii asilimia tano ambayo imekusudiwa kwenda kwa wanawake na vijana masharti yake ni rahisi sana ukilinganisha na masharti ambayo yanatolewa na taasisi za fedha kama mabenki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachoomba kumekuwa na dhana potofu kama vile fedha hizi zinatolewa kama vile ni pesa ambayo haitakiwi kurejeshwa, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba tunasimamia ili pesa hizi zinazotolewa ziweze kurejeshwa na wengine waweze kukopeshwa, vizuri tukawa na mfumo ambao ni rasmi ili kuhakikisha kila shilingi ambayo inatolewa inarudi ili wakinamama wengine waweze kukopeshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili angependa masharti ya benki yakapunguzwa ili wakina mama waweze kuna access ya kwenda kukopa kwenye taasisi hizi za fedha. Hili ambalo lipo ndani yuwezo wetu kama ofisi ya Rais TAMISEMI ni kuhusiana na asilimia tano kama ambavyo swali lake la msingi lipo ni vizuri kwanza tuhakikishe kwamba fedha hizi ambazo zinakusanywa asilimia tano inatengwa na zile zinazotengwa zinakopwa ikionekana kwamba kuna gap ya uhitaji hapo ndio twende kwenye taasisi zingine za fedha.

NAIBU WAZIRI VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sambasamba na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI ni kwamba katika mwezi huu wa tatu Mheshimiwa Rais alikaa na wadau mbalimbali wenye masuala ya kibiashara na viwanda katika moja ya jambo ambalo alizungumza ni kuwashauri watu wa mabenki kuweza kupunguza riba na kuweka masharti ambayo yatawasaidia zaidi wafanyabiashara. (Makofi)
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi naomba nimuulize Mheshimiwa naibu Waziri swali moja la nyongeza.
Kwa kuwa mfuko huu wa kina mama na vijana unatakiwa uchangiwe na maeneo mawili kwa maana ya Serikali Kuu itoe fedha kwa ajili ya ule mfuko lakini pia Halmashauri zetu zitoe asilimia 10 kwa ajili ya ule mfuko. Kwa baadhi ya Halmashauri ikiwepo Kaliua tunajitahidi sana kutenga ile asilimia 10 lakini Serikali haitoi ile sehemu yake.
Je, Serikali haioni kwamba kutokutenga ni kuendelea kudumaza wanawake na vijana kutokupata mikopo kwa kiasi kinachotakiwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la msingi lilivyo ni juu ya Halmashauri kuhakikisha kwamba wanatenga asilimia 10 na yeye katika Halmashauri yake anasema wamekuwa wakitenga hii asilimia 10 kwa uzuri zaidi.
La kwanza ambalo naomba tuhamasishe na kuagiza Halmashauri zote ni kuhakikisha kwamba wanaiga mfano mzuri kama ambavyo Halmashauri ya Kaliua inafanya ili kwanza tuwe na uhakika katika hii asilimia 10 ambayo inatengwa, je, inawafikia akina mama na baada ya hapo tukiwa na uhakika na mfumo ambao ni rasmi unatumika Serikali haitasita kwa sababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba inawakomboa wanawake na vijana na ndio maana sheria ilipitishwa ili kuhakikisha kwamba tunawawezesha wanawake na vijana katika suala zima la uchumi.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana; kwa kuwa Halmashauri nyingi sana zinakabiliwa na changamoto ya kuwa na mapato madogo na hivyo kushindwa kabisa kutenga fedha hizi za asilimia 10, asilimia tano wka vijana na asilimia tano kwa akina mama kwa ukamilifu.
Je, Serikali inachukua hatua gani kwa Halmashauri ambazo hazitengi kabisa na hata tuliona katika bajeti ya mwaka jana kuna Halmashauri mbili zilikuwa zimetajwa kwamba hazijatenga kabisa fedha hizi za akinamama na watoto, lakini hatujaona Serikali ikiwachukulia hatua. Je, Serikali inachukua hatua gani kwa Halmashauri ambazo hazitengi kabisa fedha hizi za akina mama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna excuse yoyote ambayo itasababisha Halmashauri isamehewe eti kwa sababu makusanyo yake ni kidogo. Kwa sababu hata kama ungekusanya shilingi moja, shilingi moja hiyo tunachotaka asilimia 10 ya shilingi moja si ya kwako. Wewe ni kama conduit tu unatakiwa pesa hiyo iende kwa wanawake na vijana.
Kwa hiyo, kama ambavyo tulisisitiza juzi katika jibu ambalo alijibu mwenzangu tutachukua hatua kali kwa Halmashauri yoyote na hasa Wakurugenzi wahakikishe kwamba asilimia 10 ya kutenga katika mapato ya ndani sio option, it’s a must! Na yeyote ambaye hatatekeleza hilo hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.
MHE. OMARI A. KIGODA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Handeni inahudumia karibia majimbo manne; na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amekubali hili ni suala la dharura haoni kwamba kuna umuhimu wa sisi kupata ambulance badala ya kutumia haya magari ya kawaida ambayo muda mwingi vifo hutokea njiani kwa sababu sio magari special ya kusafirisha wagonjwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba uko uhitaji mkubwa sana wa gari la wagonjwa na pia ni ukweli usiopingika kwamba uwezo wa Halmashauri kuweza kununua gari jipya kwa sasa hivi ni mdogo sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kulitambua hilo ndiyo maana Halmashauri ya Handeni imetuma ombi maalum Wizara ya Fedha ili kuomba gari la wagonjwa liweze kununuliwa. Naamini hali ya bajeti ikitengemaa ombi lao litaweza kujibiwa na wagonjwa waweze kupata gari ambalo litakuwa linamudu kwa mazingira ya Wilaya ya Handeni.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Lulindi nilitaka nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba kwa kuwa Kituo cha Afya cha Nagaga kilichopo katika Jimbo la Lulindi, Wilayani Masasi liliungua moto miaka mitano iliyopita. Je, Serikali haioni umuhimu sasa katika mgao huu wa magari yaliyopatikana kupeleka katika Kituo cha Afya cha Nagaga ili huduma za afya ziendelee kuboreka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uko uhitaji mkubwa sana wa magari ya wagonjwa. Kama ambavyo Serikali ingependa yote tukaweza kuyatatua kwa mara moja, lakini pia ni ukweli usiopingika kwamba bajeti hiyo kwa sasa haiwezekani kwa wakati mmoja tukatekeleza yote hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge ajue nia njema ya Serikali ndiyo maana katiak orodha ya Wilaya zile 27 ambazo zinaenda kujengewa Hospitali za Wilaya ni pamoja na Wilaya yake. Kwa hiyo, aelewe dhamira njema ya Serikali na kadri uwezo utakavyokuwa unajitokeza hakika hatutawasahau.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jiografia ya Jimbo na Halmashauri ya Wilaya ya Msalala wewe unaifahamu lakini pia hata Mheshimiwa Kandege anaifahamu kwamba vituo vya afya vimejengwa sana na wananchi na hivi sasa tuna vituo vya afya vitatu, cha Isaka, Ngaya na Bugarama. Lakini vituo vyote hivi havina gari la wagonjwa na kwa Halmashauri nzima gari ambalo linafanya kazi ni gari moja tu. Wananchi wamefanya kazi kubwa na wanaamini Serikali yao pia inaweza ikawashika mkono.
Kwa hiyo, nilitaka kujua Mheshimiwa Waziri unawaahidi nini wananchi hawa angalau kuwapatia gari angalau kwenye kituo kimoja katika hivi vitatu nilivyovitaja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Halmashauri za kupigiwa mfano na kama kuna Wabunge ambao wanatakiwa wapongezwe ni pamoja na Mheshimiwa Maige. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni katika Halmashauri ambazo wamejenga vituo vya afya vingi, hongereni sana. Pia nimuombe Mheshimiwa Maige kwa kushirikiana na Halmashauri yake, natambua uwezo mkubwa wa Halmashauri yake hakika wakiweka kipaumbele kama ni suala la kununua gari hawashindwi na wengine wataiga mfano mzuri ambao wao wanafanya na hasa katika own source zao ambao wanapata mapato mazuri ni vizuri katika vipaumbele wakahakikisha wananunua na gari la wagonjwa kwa ajili ya kusaidia wananchi wa Msalala.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale yenye kata 20 na kituo kimoja cha aya haina gari ya wagonjwa. Shida tuliyonayo ni kubwa sana ukizingatia mtawanyiko wa kata zetu zile pale Wilaya ya Liwale mwenyewe Mheshimiwa Naibu Waziri ni shahidi, umefika, umeona jinsi shida ya Wilaya ya Liwale ilivyo juu ya kupata gari la wagonjwa. Ni lini sasa Serikali itatupatia gari la wagonjwa katika Hospitali yetu ya Wilaya ya Liwale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika fursa nikiwa nahudumu katika nafasi ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais, TAMISEMI nimepata nafasi ya kwenda Liwale na tukakutana na Mheshimiwa Mbunge katika kazi nzima ya kujenga kituo cha afya na muitikio wa wananchi wa Liwale ni mkubwa sana katika kujitolea katika shughuli za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwa spirit niliyoiona na hakika na mapato ambayo wanapata kutokana na zao la korosho na wakasimamia vizuri kabisa mapato ya kwao na kituo kile cha afya kikikamilika hitaji la kwanza la wananchi naomba nimuagize Mkurugenzi katika vipaumbele vyake vya kwanza ni pamoja na kuhakikisha kwamba wananunua gari la wagonjwa kwa sabbau wezo upo, pesa zikisimamiwa vizuri, kulikoni kuishia kugawana kama posho hakika uhitaji mkubwa wa gari la wagonjwa wafanye kama kipaumbele.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa vile kwenye Jimbo la Mufindi Kusini Wilaya ya Mufindi, tuna ujenzi wa hospitali ambayo ni kubwa sana.
Je, Wizara ya TAMISEMI mnaweza mkatusaidia kupata ramani ambayo ni standard kwa ajili ya kujenga hospitali pale Jimbo la Mufindi Kusini?
Swali langu la pili, kama alivyoeleza kwenye majibu yako kwamba tuna ujenzi mkubwa sana pale Malangali Kituo cha Afya. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutupatia zile milioni 400; lakini kile kituo cha afya tunategemea kifunguliwe na mtu mkubwa sana. Je, Naibu Waziri uko tayari kutuunganisha na Waziri Mkuu aweze kufika pale Malangali kufungua kile kituo cha afya ili kianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Halmashauri kwa kazi nzuri waliyofanya kuhakikisha kwamba kituo cha afya kile kinakamilika na ni miongoni mwa vituo vya afya ambavyo vimejengwa kwa ustadi mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya suala la ujenzi wa hospitali ya Wilaya hitaji lake kubwa ni upatikanaji wa ramani, naomba nimhakikishie kwamba Wataalam wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Wataalam Wizara ya Afya, wako mbioni kukamilisha ramani ambazo zitatumika katika ujenzi wa Hospitali za Wilaya hizo 67 ikiwemo ya kwake ya Mufindi. (Makofi)
Swali lake la pili anaomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI imuunganishe uwezekano wa Mheshimiwa Waziri Mkuu kuwa miongoni mwa watu watakaoenda kuzindua kituo chake cha afya. Naomba nimhakikishie utaratibu unaandaliwa chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutaanza vituo 44 vyote vile ambavyo vimejengwa na kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatarajia pale Mheshimiwa Rais kwa nafasi yake na jinsi atakavyoridhia kutakuwa na uzinduzi ambao utafanyika nchi nzima tukianzia na hivyo vituo 44; sina uhakika sasa kwa nafasi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ataweza kwenda kuzindua kwake. (Makofi)
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nishukuru Serikali kwa jitihada zake za ku-support ujenzi wa vituo vya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo langu la Kwela tunavyo vituo vya afya ambavyo vimeanza kujengwa toka mwaka 2004 na wananchi wamejenga mpaka jengo la OPD kukamilika, lakini vituo hivyo mpaka sasa vimesimama kwa sababu havijapata fedha tena. Vituo hivyo ni Kituo cha Ilemba, Kahoze na Muze.
Je, ni lini Serikali itatoa fedha ku-support wananchi juhudi zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anauliza ni lini Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kumalizia vituo vya afya ambavyo vimeanzishwa na wananchi muda mrefu.
Kwanza naomba nimtaarifu kwamba nia njema ya Serikali ya kuhakikisha kwamba huduma ya afya inafika kila mahali ikiwa ni pamoja na Wilaya yake, katika hospitali 67 ambazo zinaenda kujengwa za Wilaya na Wilaya yake ni miongoni mwa hospitali ambazo zitaenda kujengwa. Hiyo ni nia njema ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma inapelekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na hivyo vituo vyake kama nilivyojibu kwenye swali la msingi pale pesa inapopatikana hakika naomba nimhakikishie na hii itakuwa miongoni mwa vituo vya afya ambavyo vitaboreshwa ili viweze kutoa huduma tunayoitarajia.(Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wafanyabiashara kote nchini hivi sasa wanalalamika biashara zao kuyumba na ukweli uliopo ni kwamba tatizo hili bado linaendelea katika Manispaa hii ya Mpanda. Je, Serikali iko tayari kuiagiza Halmashauri kwa spirit ya utawala bora kukaa tena na wafanyabiashara hawa ili kuweza kwa pamoja kujadili kiwango ambacho Halmashauri na wafanyabiashara watanufaika ili sasa pande zote mbili ziweze kufanya kazi bila manung’uniko?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika utendaji bora na ushirikiano na Halmashauri ni kwamba maeneo mengi utendaji unaonekana kukwama kwa sababu wakati mwingine mabavu yanatumika katika kuweka hivi viwango vya kodi na kadhalika. Ni lini Serikali itatoa maagizo ya hakika kabisa ili Halmashauri zisigombane na wateja wao ambao ni hawa wafanyabiashara na sasa hivi tunavyohimiza Halmashauri ziweze kuongeza vyanzo vipya vya mapato ili mapato ya Serikali kokote katika nchi yetu yasipotee tu kwa sababu ya uhusiano mbaya kati ya Halmashauri pamoja na wafanyabiashara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nafarijika swali kama hili kutoka kwa Mheshimiwa Selasini na bahati nzuri yeye ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na TAMISEMI. Katika nafasi niliyopata kushiriki katika vikao vyake amekuwa akihimiza Halmashauri zihakikishe kwamba zinakusanya mapato yake ili ziweze kujiendesha.
Mheshimiwa Spika, umenisaidia. Sisi Waheshimiwa Wabunge ni Madiwani tukiwa kwenye halmashauri zetu. Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ilishirikisha wafanyabiashara, zimeundwa Tume zisizopungua tatu na katika jibu langu la msingi nimeeleza hawa ambao wamekuwa wanapangishiwa wamekuwa wakilipa Sh.100,000 mpaka Sh.150,000.
Mheshimiwa Spika, sasa halmashauri katika kuona katika vyanzo vyao ambavyo ni vizuri wakavisimamia iko katika kupandisha kutoka Sh.15,000 ambayo imekuwa ikitozwa zaidi ya miaka 30 na kwenda mpaka Sh.40,000 which is very fair.
Mheshimiwa Spika, ameelezea juu ya suala zima la kutokuwa na migongano baina ya wafanyabiashara na halmashauri. Kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi, ushirikishwaji umekuwepo na hata ninavyoongea leo hakuna hata kibanda kimoja ambacho kimefungwa katika Manispaa ya Mpanda kwa sababu ushirikishwaji umekuwepo. Zimekuwepo Tume zaidi ya tatu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba maridhiano yanakuwepo na halmashauri inapata chanzo chake cha pesa na kinatumika sahihi.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Siha inafanana na wilaya iliyotajwa hapo lakini kwa tofauti kidogo, Halmashauri ya Siha ina magulio, haina masoko. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano alishatoa maelekezo kwamba akinamama wanaotandaza bidhaa chini na wale ambao ni wa chini kabisa wasidaiwe ushuru.
Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha kabisa jana katika Wilaya ya Siha wananchi kwenye soko la Sanya Juu wameenda kulazimishwa kulipa ushuru kwa kutumia polisi na wananchi waliposema Rais alishasema sisi tunaotandika chini tusilipe waliambiwa Rais huyo huyo ndiye anasema tukusanye kodi na bado yeye anatuvuruga kwenye kukusanya kodi, lipeni ushuru na polisi wakapelekwa sokoni na wananchi walipata taharuki sana.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba nielezwe kwamba tunawezaje kuwasaidia hawa akinamama ambao ni vipenzi vya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari alishatoa maelekezo na yamekuwa yakipuuzwa na Halmashauri zetu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, maelekezo aliyotoa Mheshimiwa Rais kwamba wale akina mama ambao wanapanga bidhaa zao ikiwa ni pamoja na wale ambao wanauza ndizi wasibugudhiwe ni msimamo ambao uko thabiti, hauyumbi hata mara moja. Kama kuna Mkurugenzi yeyote ambaye hataki kutekeleza kauli na maelekezo ya Mheshimiwa Rais tafsiri yake ni kwamba Mkurugenzi huyo hajitaki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie, leo wakati naingia nilimwambia Mheshimiwa Mollel katika maeneo ambayo nina wajibu wa kwenda kutembelea ni pamoja na Jimbo lake hii ni pamoja na kwenda kutazama eneo la ujenzi wa hospitali mpya ya wilaya. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, katika Hospitali ya Wilaya ya Kasulu kuna upungufu mkubwa wa Madaktari na Wauguzi, Muuguzi mmoja anahudumia wodi moja akiwa peke yake hali inayosababisha azidiwe na shughuli. Wagonjwa wanawalalamikia Wauguzi kwamba hawawahudumii lakini ni kutokana na kuzidiwa na kazi nyingi. Je, ni lini Serikali itapeleka Waganga na Wauguzi ili kumaliza tatizo liliko katika Wilaya ya Kasulu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, katika Mkoa wa Kigoma kuna kambi tatu za wakimbizi. Wilaya ya Kasulu kuna Kambi ya Nyarugusu, Wilaya ya Kakonko kuna Kambi ya Mtendeli na Wilaya ya Kibondo kuna Kambi ya Nduta. Wagonjwa wanapozidiwa katika kambi mbili ya Mtendeli na Nduta katika Wilaya ya Kibondo na Kakonko, wale wa Nduta hupelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kibondo na wale wa Mtendeli hupelekwa katika Kituo cha Afya cha Kakonko. Je, ni lini Serikali, kwanza, itapeleka pesa za kumalizia Hospitali ya Wilaya katika Wilaya ya Kakonko na kupeleka Wauguzi na Madaktari? Pili, katika Wilaya ya Kakonko ni lini nao watapelekewa Waganga na Wauguzi wa kutosha ili kumaliza matatizo yaliyopo katika hospitali hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) :
Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimekiri upungufu wa waganga pamoja na watumishi wa afya kwa ujumla wake. Pia nimeeleza jinsi ambavyo katika bajeti ya 2018/2019 walivyoomba kupatiwa Waganga 1,667.
Mheshimiwa Spika, lakini ni nia njema ya Serikali ya kuhakikisha kwamba huduma ya afya inatolewa. Nimepata nafasi ya kwenda Kasulu na tatizo ambalo nimekutana nalo pale Kasulu ni pamoja na kutokuwepo vituo vya afya vya jirani ili hospitali ya wilaya iwe na sehemu ya kupumulia. Katika utaratibu mzima wa Serikali wa kuhakikisha kwamba huduma ya afya inapatikana ya kutosha. Miongoni mwa wilaya 67 ambazo zinaenda kupata hospitali za wilaya, Wilaya za Kigoma zitakuwepo ikiwa ni pamoja Uvinza, Buhigwe pamoja na Kasulu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, Kakonko kuna Kituo cha Afya kinaitwa Gwamanumbu na Lusesa nao wanaenda kupata kituo cha afya ambacho kina hadhi ya kuweza kufanya operesheni. Hii yote kwa ujumla wake unaona jinsi ambavyo Serikali ina nia njema ya kuhakikisha kwamba afya kama jambo la msingi linaenda kupatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Waziri wa Utumishi na Utawala bajeti yake imesomwa jana na sisi TAMISEMI pamoja na uhitaji wetu kibali cha ajira tunapata kutoka kwao. Naamini katika maombi haya ya wahudumu pamoja na Waganga 1,667 tutapata wa kutosha na tutaenda kupunguza huo uhaba wa watumishi.
Mheshimiwa Spika, yeye mwenyewe ni shuhuda kwamba kuna mashirika ambayo yamekuwa yakishirikiana na Serikali kwa sababu suala la wakimbizi huwezi uka-predict kwamba watakuja wangapi. Naamini kwa ushirikiano ambao umekuwa ukioneshwa hakika huduma ya afya itaenda kuboreshwa na tatizo hili litapungua.
MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Katika Kamati yetu ya huduma za jamii ni wazi kwamba tuna upungufu wa watumishi wa afya takribani 48%. Katika zoezi hili la uhakiki vituo vingi vya afya vimefungwa, hali inayosababisha akinamama wengi wajawazito kuendelea kufariki na hata takwimu zinaonesha kwamba wanaokufa ilikuwa 400 na zaidi kati ya vizazi 100,000 leo tunaongelea zaidi ya wanawake 500 na zaidi katika vizazi 100,000.
Mheshimiwa Spika, ni kwa nini sasa Serikali haiajiri wakati Madaktari wako kibao na watumishi hao wako nje ya ajira? Ni kwa nini Serikali haiajiri wakati watu wetu wanaendelea kufariki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) :
Mheshimiwa Spika, tumekiri juu ya upungufu wa wataalam wa afya lakini pia ni ukweli usiopingika kwamba unapoajiri implication yake ni suala la bajeti. Naamini kabisa kwa upungufu huu tulionao na idadi ya watumishi katika kibali ambacho kimetoka wanaoenda kuajiriwa ni pamoja na Madaktari. Naomba tuvute subira tupitishe bajeti hii wengi wa wale wanaoenda kuajiriwa itakuwa ni Madaktari ili kupunguza tatizo hili kubwa tulilonalo.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, naomba nimuulize swali dogo tu la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyopo huko Mkoani Kigoma yapo pia katika Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, kuna uhaba mkubwa wa watumishi, vituo vya afya na zahanati wakati mwingine vina mtumishi mmoja. Je, Serikali iko tayari sasa baada ya kuajiri kuleta watumishi katika Halmashauri ya Itigi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika wale watumishi watakaokwenda kuajiriwa hakika tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba sehemu ambayo kuna upungufu mkubwa ikiwa ni pamoja na jimbo lake tunawapeleka.
Mheshimiwa Spika, wakati Mheshimiwa Susan anaongea, aliongelea kuhusiana na baadhi ya vituo kufungwa na sisi Wabunge ni mashuhuda Mheshimiwa Waziri wa Utawala Bora alitoa tamko tukiwa humu ndani ya Bunge kwamba kama kuna eneo lolote Mbunge anajua kwamba kituo kimefungwa kwa sababu ya kukosekana watu wa kutoa huduma pale apeleke maombi ili isitokee hata sehemu moja eti tumefunga kituo kwa sababu hakuna mtu wa kutoa huduma ya afya kwa eneo husika.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kuwasihi Waheshimiwa Wabunge kama kuna maeneo ambayo tumejenga na Mheshimiwa Bobali alisema jana, ni fursa hii tuhakikishe kwamba hakuna kituo cha afya hata kimoja au zahanati yetu hata moja ambayo inajengwa ikakamilika ikaacha kutumika eti kwa sababu hakuna watu wa kutoa huduma.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza naomba niishukuru Serikali kwa kuitupia sekta ya afya jicho la pekee katika Jimbo langu la Ulanga. Kituo cha Afya cha Lupilo karibu kinakwisha, sasa wananchi wa Ulanga wategemee nini katika huo mgawo? Siyo kwamba Madaktari ni wachache tu lakini ni pamoja na kuwa na watumishi wa afya wasio na sifa. Ulanga inakusikiliza sasa hivi Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ulanga limepewa kipaumbele sana kwenye sekta ya afya, hilo naishukuru Serikali, hicho ndiyo kipaumbele cha Mbunge wao, kipaumbele cha kwanza afya, cha pili afya, cha tatu afya. Shida kubwa iliyopo ni watumishi wachache, Mheshimiwa Waziri katika majibu yake haya ya kugawa watumishi wa afya wananchi wa Ulanga wanamsikiliza sasa hivi anawaambia nini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba nitangulie kupokea shukrani anazozitoa, lakini naomba nimhakikishie nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba vituo vya afya na zahanati zetu zote zinafanya kazi iliyokusudiwa kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika, litakuwa ni jambo la ajabu tukamilishe kituo cha afya kizuri halafu kisiwe na watenda kazi. Katika wilaya ambazo zitapata watendaji kwa maana ya wahudumu wa afya pamoja na Waganga, nimhakikishie kwamba wale wenye sifa ndiyo ambao watapelekwa kwake, kwa hiyo, wananchi wategemee mambo mazuri kuhusiana na suala zima la afya.
MHE. SAUL H. AMON: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Naomba kama Naibu Waziri ana nafasi aone hali ilivyo mbaya, kile kipande cha kata nne hata kwenda kuwasalimia tunaogopa kwa sababu tunatoa ahadi lakini haitimizwi. Je, yuko tayari kuongozana na mimi akaangalie hali ilivyo mbaya ya hicho kipande cha kutoka Njiapanda mpaka Mpakani? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, vilevile barabara hii iko sawa kabisa na barabara ya Igogwe – Mchangani - Mbeye One. Mazao ni mengi lakini wananchi wa eneo hilo wanauza mazao kwa bei ya chini sana kwa sababu hakuna usafiri. Naomba Waziri atakapokuja Rungwe aangalie vipande hivyo viwili na aone ukweli na hali halisi ilivyo kwa wananchi wa Rungwe. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kubwa ambalo Mheshimiwa Mbunge analitaka kwangu mimi ni suala la kupata fursa ya kwenda kutembelea ili nijionee kwa macho hali halisi ikoje. Mimi niko tayari baada ya kwamba tumehitimisha shughuli za Bunge la Bajeti, nikiamini kwamba bajeti yetu itakuwa imepita salama ili nikajionee na tushauriane.
Mheshimiwa Spika, lakini pia naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kupitia chombo chetu cha TARURA ambacho tumekianzisha tutahakikisha tunawaelekeza maeneo yote ambayo ni korofi yaweze kutengenezwa ili yapitike vipindi vyote.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Barabara ya kutoka Ilunda - Igongolo yenye kilometa tisa ni ya TANROADS na imetengenezwa lakini mbele inaendelea kwenda Kivitu – Kifumbe – Makambako urefu wa kilometa 19 na tuliomba ipandishwe hadhi. Ni lini Serikali itaipandisha hadhi barabara hii kuwa ya TANROADS ili itengenezwe iweze kuzunguka kama ambavyo imefanyika kwa zile kilometa 9?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, sisi sote ni mashuhuda tukiwa katika Bunge lako Tukufu Wabunge wengi walikuwa wakiomba barabara zao zipandishwe hadhi na zichukuliwe na TANROADS. Mawazo hayo Bunge lako Tukufu likachukua na kulifanyia kazi kwa nini Wabunge wengi tumekuwa tukiomba barabara zichukuliwe na TANROADS?
Mheshimiwa Spika, jibu ni jepesi kabisa kwamba kwa sababu barabara ambazo ziko chini ya TANROADS zimekuwa zikitengenezwa kwa kiwango kizuri. Ndiyo maana tukasema tuanzishe chombo ambacho kitakuwa kinafanya kazi nzuri kama TANROADS wanavyofanya na ndiyo essence ya kuanzishwa kwa TARURA.
Mheshimiwa Spika, naomba tutoe fursa kwa chombo hiki ambacho tumekianzisha ndani ya Bunge lako kifanye kazi. Naamini kinafanya kazi nzuri kwa sababu tumeanza kupata taarifa kutoka kwa baadhi ya Wabunge, wengi wana- appreciate jinsi ambavyo TARURA imeanza kufanya kazi. Naamini hata Mheshimiwa Mbunge kilio chake si barabara kuchukuliwa na TANROADS bali barabara itengenezwe ipitike kwa vipindi vyote.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri mapema mwaka huu alifanya ziara katika Halmashauri yetu ya Mji wa Babati nasi tukakueleza juu ya ahadi ya Mheshimiwa Rais kuhusu ujenzi wa barabara za lami kilometa 20 alizoahidi wakati wa kampeni. Wananchi wa Babati wanauliza ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kilometa 20 za lami katika Mji wao wa Babati utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli nilipata fursa ya kutembelea Babati, lakini pia katika ziara yangu sikumbuki kama Mheshimiwa Gekul alisema hilo. Hata hivyo, kwa sababu ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na ahadi zake ni mkataba baina yake yeye na wapiga kura na mkataba huu ni ndani ya miaka mitano, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, yale yote ambayo yameahidiwa na Mheshimiwa Rais yanaratibiwa na ndani ya miaka mitano yataweza kutekelezwa.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi hii muhimu sana. Kutokana na mvua ambazo zinaendelea kunyesha barabara nyingi za Jimbo la Kaliuwa zimekatika na hazipitiki kabisa, zikiwemo barabara ambazo zinatoa magari Kahama kwenda Kaliuwa na kwenda vijiji mbalimbali. Barabara ya Kahama kwenda Ugaza imekatika, Kahama kwenda Usinge imekatika, Usinge kwenda Lugange Mtoni imekatika na Kahama kwenda Mpanda Mloka imekatika.
Mheshimiwa Spika, TARURA waliomba bajeti ya dharura ili waweze kufungua barabara hizi ambazo sasa hivi hazipitiki kabisa, wananchi wametengeneza mitumbwi ya kupita. Naomba Serikali ituambie mpango wa haraka wa kuweza kuwapa fedha kwa TARURA, Wilaya ya Kaliuwa ili waweze kutengeneza barabara hizi ziweze kupitika kwa sababu ni barabara kubwa za uchumi? Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kuhusu suala la barabara nyingi kukatika kwa sababu ya mvua zinazonyesha, naomba nimhakikishie na itakuwa vizuri mimi nikishatoka baada ya hapa tukafanya mawasiliano ili tuhakikishe haraka kabisa barabara hizo zinatengenezwa ili ziweze kupitika. Kwa sababu ni lengo la Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote zinapitika kwa vipindi vyote.
Mheshimiwa Spika, ametaja barabara nyingi, itapendeza kama tutawasiliana halafu tuone jambo gani la haraka linaweza likafanyika ili wananchi wasije wakakwama katika shughuli zao.
MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Tatizo la barabara katika Jimbo la Songea Mjini hususan barabara itokayo Songea Mjini kupita Kata ya Ruvuma na Kata ya Subira ni kubwa sana kiasi kwamba haipitiki na hata mimi Februari hii nilikwama wakati natumia barabara hiyo. Je, Mheshimiwa Waziri ni lini barabara hiyo itaweza kutengenezwa kwa kiwango cha lami ili kuwahudumia wananchi wa Jimbo la Songea Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni lini barabara hiyo itaweza kutengenezwa kwa kiwango cha lami, najua kiu yake kubwa angetamani hata kesho barabara ikakamilika, lakini ni ukweli usiopingika kwamba kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami inahitaji pesa za kutosha.
Mheshimiwa Spika, hivyo, ni vizuri katika vipaumbele vya halmashauri yake na katika vyanzo vya mapato walivyonavyo wakaweka kama ni kipaumbele. Pia ni vizuri nikipata fursa wakati nikiwa katika ziara kwenda Ruvuma nitapita ili tushauriane na Mheshimiwa Mbunge tukiwa site ili tuone umuhimu wa barabara hii.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo ya nyongeza, lakini naomba nitumie nafasi hii kuwapa pole wananchi wangu wa Jimbo la Nyang’hwale kwa mauaji ya kikatili ambayo yamefanyika wiki iliyopita, akina mama wanne wamenyongwa kwa kutumia kanga zao na wawili wakiwa wajawazito na mauaji hayo yanaendelea kwa Wilaya za jirani.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali dogo la nyongeza ni kama ifuatavyo; je, Serikali ina mpango gani wa kutoa fedha kuisaidia Halmashauri ya Nyang’hwale ili kukamilisha ujenzi wa zahanati iliyopo Iyenze na Mwamakiliga? Serikali ina mpango gani kuisaidia Halmashauri?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, naishukuru AMREF kwa kukamilisha majengo matatu yaliyopo pale Kituo cha Afya Kharumwa. Serikali ina mpango gani baada ya kukamilishwa majengo hayo kuendeleza kwa kutusaidia kuongeza vifaatiba pamoja na wauguzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa jitihada zake za kuhakikisha wananchi wanapata huduma iliyo bora ya afya. Yeye hakika ni mfano bora wa kuigwa kwa Waheshimiwa Wabunge wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza, anauliza Serikali kusaidia Halmashauri kumalizia zahanati, ni nia ya dhati kabisa ya Serikali kuhakikisha kwamba tunasaidia, lakini kinachogomba ni uwezo. Kwa hiyo, kadri bajeti itakavyokuwa imeboreka, hakika hatuwezi tukawaacha wananchi ambao Mheshimiwa Mbunge ameonesha jitihada tukaacha kumalizia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili baada ya kazi nzuri iliyofanywa na AMREF, suala la zima la kupeleka vifaa pamoja na wataalam, ili kazi iliyotarajiwa iweze kuwa nzuri, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vya afya na zahanati zetu zote zinafanya kazi. Muda siyo mrefu, wakati tunahitimisha, Mheshimiwa Waziri wa Utawala atakuja kusema neno kuhusiana na suala zima la kuajiri watumishi wa Serikali. (Makofi)
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Mtikila kilijenga zahanati ambayo ilikamilika mwaka 2015, lakini mpaka leo haijafunguliwa kwa sababu ya tatizo la vifaa na wataalam. Namuomba Naibu Waziri aniambie, ni lini watafungua zahanati hii ili kutokudhoofisha nguvu za wananchi?
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tulipokea katika michango ya Mheshimiwa Bobali na nikayarudia katika moja ya maswali ambayo nilikuwa najibu hapa, kwamba ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba zahanati ambazo zimekamilika huduma itatolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimetangulia kusema muda siyo mrefu kwamba ni siku ya leo ambapo Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Utawala atakuja kuhitimisha na atasema neno kuhusiana na suala zima la kupatikana wahudumu wa afya na waganga, maana na sisi tunategemea kupata kibali cha ajira kutoka kwake.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira yaliyopo Jimbo la Nyang’hwale yanafanana kabisa na mazingira yaliyopo kwenye Jimbo la Ndanda na hasa kwenye Kata ya Chiwata ambapo kuna Shule ya Sekondari ya Chidya. Wananchi wa Chidya waliamua wenyewe kutumia nguvu zao kujenga jengo pale kwa ajili ya kuweza kupata zahanati. Kwa bahati mbaya kabisa, maelekezo niliyokuwa nawaambia, watakapokuwa wamefanikiwa kukamilisha boma, wawe wameendelea juu wameweka mpaka bati, Serikali itakuja kumalizia kuwaletea vifaa pamoja na kufungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri ya kututaka tusubiri, lakini napenda watu wale wasikie, Chidya ni sehemu ya mkakati wa hiyo mikakati yenu ya Wizara kukamilisha maboma hayo na lini hiyo kazi itafanyika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali na pia ni azma ya CCM; ukisoma katika Ilani ya CCM ukurasa wa 81 Ibara ya 50 tumetaja kabisa kwamba kila sehemu ambayo ipo kijiji tutahakikisha kwamba inajengwa zahanati, kila Kata itakuwepo na Kituo cha Afya na kila Wilaya itakuwa na Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, ni azma thabiti na ndiyo maana imeandikwa. Naomba nimweleze Mheshimiwa Mbunge avute subira.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge amesema kwamba wananchi wake kama ilivyo Nyang’hwale wamejitolea, lakini sina uhakika kama naye Mheshimiwa Mbunge amefanya kazi nzuri kama Mbunge wa Nyang’hwale. Na yeye tumtake ashirikiane na Serikali, kwani wanaotibiwa ni wananchi wetu. Kwa hiyo, ni vizuri wote tukashiriki katika suala zima la kuhakikisha kwamba afya inakuwa bora. (Makofi)
MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza nipongeze kazi nzuri ya kuboresha mazingira ya kutolea afya katika maeneo yetu kwa nchi nzima. Kutokana na shida kubwa ya afya iliyopo katika maeneo yetu tuliyokuwa nayo, Serikali ije na mpango mahususi wa kuhakikisha kwamba zile nguvu za wananchi katika maeneo yote waliyojenga maboma ya zahanati na nyumba za wauguzi, inawasaidia kumaliza maboma hayo. Je, Serikali lini itafanya hilo ili kumaliza shida ya afya katika maeneo yetu? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, mpango mahususi wa Serikali upo na ndiyo maana katika bajeti hii ambayo tunakwenda kumaliza, jumla ya vituo 208 vinaenda kujengwa, lakini pia katika bajeti ambayo ndiyo tunaomba Waheshimiwa Wabunge leo wapitishe, nina uhakika kwamba ikipitishwa jumla ya shilingi bilioni 100.5 inaenda kutumika kwa ajili ya kujenga Hospitali za Wilaya 67 katika Halmashauri zetu. Hiyo yote inaonesha dhamira ya Serikali kwamba ina nia ya kuhakikisha kwamba tatizo la afya linaondolewa.
MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu suala hili, bahati nzuri mwenyewe anayezungumza ni ametoka Mkoa wa Rukwa, kwa hiyo, barabara hii anaifahamu vilivyo. Akina mama wengi na watoto wanapata shida kwenye barabara hii wanapokuja kupata huduma ya afya Namanyere.
Napenda kuiuliza Serikali, je, ina mpango gani kwa hivi sasa kwa sababu tupo katika kipindi cha bajeti kuweza kutenga fedha za kutosha kuikamilisha hii barabara badala ya kuendelea kutengeneza maeneo korofi kila mwaka hadi mwaka na kuonekana kana kwamba ni mradi wa Serikali? (Makofi)
Swali la pili, ninapenda kuiomba Serikali ijaribu kuona hizi barabara zetu za Bonde la Lake Tanganyika na Bonde la Lake Rukwa, barabara hizi ni tata, zinahitaji matengenezo yaliyokamili kama vile Kitonga na inavyoelekea kutumika katika kipindi chote cha mwaka mzima.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba barabara hii ina changamoto kubwa maana kuna maeneo ambayo kuna milima mikubwa sana na azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wa Ninde wanapata barabara inayoweza kupitika kwa vipindi vyote.
Mheshimiwa Spika, kabla ya hapo ilikuwa hakuna barabara kabisa na ndiyo maana Serikali kwa kulitambua hilo ikaanza kutenga kiasi cha shilingi milioni 350 na maeneo yaliyokuwa korofi zaidi ilikuwa ni maeneo ya madaraja. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ilimradi madaraja yameshajengwa ambayo ndiyo yalikuwa ni changamoto kubwa sana, nia na azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba maeneo yaliyobaki yataweza kutengenezwa kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu.
Katika swali lake la pili, ameongelea Ukanda wa Ziwa Rukwa. Sifa ya Ukanda wa Ziwa Rukwa na hii barabara aliyoitaja ya kwenda Ninde hazina tofauti sana na Mbunge, Mheshimiwa Malocha amekuwa akiipigia kelele sana na kwa mara ya kwanza Serikali imesikia kilio chake na barabara hii inaweza kuimarishwa ili iweze kupitika katika kipindi chote.
MHE. MUNDE A. TAMBWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kutuletea pesa kwenye Wilaya ya Sikonge, Nzega na Uyui kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya, naishukuru sana Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza swali langu la kwanza la nyongeza. Ukizingatia population ya Wilaya ya Tabora Manispaa, ukizingatia Sera ya Serikali yetu kwamba mnatakiwa muanze ninyi wenyewe na Serikali iwa-support kitu ambacho wananchi wa Tabora Manispaa wameshakifanya. Kinachotushangaza zaidi ni pale Wilaya mpya zilizoanza mwaka jana zinavyopelekewa pesa ya kujenga Hospitali ya Wilaya na kuacha kupeleka katika Wilaya za zamani…
MHE. MUNDE A. TAMBWE: zenye watu wengi na…
MHE. MUNDE A. TAMBWE: ...kuacha kupeleka kwenye Wilaya ya Tabora Manispaa. Je, Serikali inanipa commitment gani sasa ya kuleta pesa kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Tabora Manispaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Jimbo la Igalula halina hata zahanati moja wala kituo cha afya kimoja; hii inasababisha wananchi wote wa Jimbo hilo kwenda kwenye hospitali kubwa ya Mkoa wa Tabora ambayo ni Kitete na kuongeza msongamano mkubwa. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha inaleta pesa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na kumalizia zahanati ambazo zilianzishwa na wananchi wa Jimbo la Igalula pamoja na Mbunge wao na mimi Mbunge wao wa Viti Maalum? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika tangu nimeingia Bunge hili na Mheshimiwa Munde akiwa ndani ya Bunge hili amekuwa ni mpiganaji kuhusiana na suala zima la afya kwa Mkoa wake wa Tabora, nampongeza sana kwa jitihada zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake mawili, swali la kwanza anauliza commitment ya Serikali katika kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa hospitali ya Manispaa ya Tabora kwa maana ya hospitali ya wilaya. Katika jibu langu la msingi nimemweleza commitment ya Serikali kwamba katika awamu ya pili, fedha zitakazopatikana kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya hatutaisahau Manispaa ya Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaongelea kuhusiana na Igalula ambayo hawana kituo cha afya na Hospitali ya Wilaya. Kwanza naomba niwaase na niwaombe wananchi wa Igalula, wao waanzishe ujenzi kama ambavyo Manispaa ya Tabora wamefanya na pesa ikipatikana awamu itakayofuata na sisi kama Serikali tutahakikisha kwamba tunaunga mkono juhudi za wananchi. (Makofi)
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kambi ya Simba Wilayani Karatu umekamilika kwa ufanisi mkubwa na kituo hicho sasa kiko tayari kuanza kutoa huduma. Hata hivyo, kituo hicho hakina gari la wagonjwa na ukizingatia Wilaya ya Karatu haina hospitali ya wilaya, je, ni lini Serikali italeta gari kwa ajili ya huduma ya wagonjwa kwenye kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunashukuru kwa kazi nzuri ambayo mwenyewe ana-recognise kwamba kituo cha afya kimekamilika na kiko kwenye hali nzuri. Hatua inayofuata anaomba upatikanaji wa gari la ambulance ili kuweza kusaidia huduma ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba uhitaji wa gari kwa ajili ya wagonjwa ni mkubwa sana. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kadri nafasi zitakavyopatikana, tulipata magari 50 na tumeweza kuyagawa, tukipata gari nyingine naamini na wao watakuwa miongoni mwa maeneo ambayo yatapata fursa ya kupata magari.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pia nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali yetu ya Wilaya iliyopo katika Manispaa ya Iringa ilifunguliwa ili kupunguza msongamano mkubwa uliyopo katika hospitali ya mkoa, lakini hospitali ile mpaka sasa hivi haina jengo la vipimo, haina wodi za wagonjwa wengine ina wodi za wazazi na hospitali ile imekuwa ikisaidia wagonjwa wanaotoka katika Wilaya ya Kilolo, Iringa DC na kwingineko; na Mheshimiwa Jafo tunamshukuru alifika; je, Serikali sasa inasaidiaje pamoja na kuwa imetoa pesa kwa ajili ya kujenga hospitali za wilaya nyingine wakati bado hazijajengwa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba ukienda Manispaa ya Iringa na kwa kuanzia hospitali ya mkoa ina wagonjwa wengi sana, ndiyo maana Serikali katika kuhakikisha kwamba tunapunguza mlundikano wa wananchi kwenda kutibiwa katika hospitali ya mkoa, ikawa ni wajibu kuhakikisha kwamba inajengwa hospitali ya wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama anavyotoa maelezo kwamba ile hospitali ya wilaya haijakamilika kwa kiwango ambacho kilitarajiwa, naomba nimhakikishie, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za wilaya ambazo zinajengwa zinakuwa katika kiwango ambacho tunakitarajia ili mwananchi akipata rufaa kutoka kituo cha afya akienda kutibiwa kwenye hospitali ya wilaya apate matumaini kwamba nimefika katika hospitali ambayo hakika kwa majengo na huduma ataweza kupona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie, kwa kadri bajeti itakavyokuwa imeruhusu tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba suala la afya ni kipaumbele kama Serikali ilivyoelekeza.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Mbulu, kwanza kuishukuru sana Serikali kwa ujenzi wa Vituo vya Afya vya Daudi na Tlawi katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu na Kituo cha Afya cha Dongobeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba pamoja na shukrani hizi ninazotoa, naishukuru pia Serikali kwa kutenga fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mbulu ambayo iko kwenye Halmashauri ya Mji wa Mbulu takribani shilingi bilioni moja na nusu katika bajeti ya mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu mawili sasa; upungufu huu wa watumishi umepelekea watumishi waliopo kufanya kazi ya ziada kutokana na kwamba hospitali hii ya Halmashauri ya Mji wa Mbulu iko mpakani mwa Halmashauri ya Babati, Halmashauri ya Karatu na Halmashauri ya Mbulu Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapokea huduma wa afya katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbulu, karibu asilimia 30 wanatoka kwenye maeneo ya pembezoni, hali inayopeleka watumishi walioko kufanya ya ziada.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Serikali iniambie inachukua hatua gani sasa kuongeza fedha za OC kwa ajili ya wale watumishi wanaofanya kazi ya ziada ili waweze kuwahumia wananchi wetu wanaotoka ndani ya Halmashauri ya Mbulu na Halmashauri nyingine za jirani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa sasa fedha zinazotengwa za dawa na vifaa tiba ni kidogo kulingana na idadi ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini na kwa kuwa wale wanaotoka nje ya Jimbo la Mbulu Mjini hawapo kwenye mpango huu; Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka sasa wa kutazama takwimu ya wananchi wanaopokea huduma ya Afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazipokea pongezi alizotoa kwa kazi ambayo inafanywa na Serikali, lakini ameuliza maswali mawili. La kwanza ni suala zima la kutoa allowance kwa wale watumishi wachache ambao wanalazimika kufanya masaa ya ziada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba kila Mtumishi na hasa wa sekta ya afya pale anapofanya kazi masaa ya ziada, ndiyo maana kuna kipengele cha on-call allowance ili waweze kulipwa stahili zao na wahakikishe kwamba wanafanya kazi ya kuwatumikia Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeomba kibali cha kuweza kuwaajiri watumishi 25,000. Kibali hiki kitakapokuwa kimepatikana ni imani yangu kubwa Hospitali yao ya Mbulu nayo itapata watumishi kama ambavyo ameomba watumishi 91, ni ukweli usiopingika kwamba itapunguza uhaba uliojitokeza kufikia sasa hivi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa matatizo ya Mbulu yanafanana kabisa na Halmashauri ya Mji wa Mafinga ambao kwa juhudi za wananchi pamoja na Serikali tunatarajia kukamilisha Kituo cha Afya cha Ulole, Kisada na Bumilahinga na pia Kituo cha Afya cha Ihongole kufuatia kupewa fedha shilingi milioni 500 na Serikali; lakini kwa kuzingatia kuwa Hospitali Mafinga iko kandokando ya barabara kuu na kati ya Iringa na Makambako hakuna hospitali hapo katikati.
Je, Serikali iko tayari kutuongezea idadi ya Watumishi ili tutakapofungua Zahanati na Vituo vya Afya hivyo, ufanisi wa kukaribisha huduma za afya kwa wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga uwe wa dhati na wa vitendo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, na wewe ni shududa kwamba wakati tunapitisha bajeti yetu Mheshimiwa Mbunge Cosato Chumi alikiri kabisa kwamba sasa hivi Mafinga ni motomoto kwa sababu kuna upanuzi wa hospitali. Pia hali iliyoko Mafinga ukilinganisha na Mbulu kuna utofauti mkubwa, maana wenzetu wana kituo. Kwanza kuna Chuo ambacho kinafundisha Waganga pale. Kwa hiyo, wakati wa kwenda kufanya practical inakuwa rahisi kwa wao kwenda katika Zahanati na Vituo vya jirani ikiwa ni pamoja Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vyote na Zahanati zote zinakuwa na wahudumu kwa maana ya Waganga pamoja na Wauguzi ili hicho ambacho kimekusudiwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma kwa wananchi kinakuwa kweli na siyo nadharia.
MHE. HAWA B. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pamoja na majibu ya Serikali ya utengaji wa maeneo, lakini je, mpaka sasa ni waombaji wangapi ambao tayari wameshapewa maeneo hayo kwa ajili uwekezaji wa viwanda vya kuchakata korosho? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mkoa wa Tabora ni moja kati ya Mikoa ambayo inalima tumbaku kwa wingi; je, ni lini Serikali itatenga maeneo ya uwekezaji wa viwanda vya korosho/ulimaji wa tumbaku ili wakulima wetu waweze kunufaika na tumbaku yao? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, anauliza ni wangapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaungana na mimi kwamba suala la kitakwimu linahitaji kupata data mapema. Namwomba Mheshimiwa ili apate jibu la uhakika, angeleta kama swali la msingi ili tuweze kumtafutia takwimu ili tumpe majibu ambayo yanastahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya Mkoa wa Tabota kutenga eneo kwa ajili ya wakulima wa korosho; kasema korosho na wakati mwingine kasema tumbaku, sasa I am not so sure ni kwa ajili ya nini? Kwa sababu hata ukienda Tabora pia korosho zinastawi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama msingi ni kwa ajili ya wakulima wa tumbaku, namwomba Mheshimiwa Mbunge na bahati nzuri yeye ni Diwani katika eneo lake, mchakato ni vizuri ukaanzia kwenye Halmashauri, maana yeye analifahamu vizuri eneo la Mkoa wa Tabora ili wahakikishe kwamba maeneo kwa ajili ya wajasiriamali yanawekwa na yanatunzwa ili watu wetu waweze kupata maeneo hayo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Majibu ya Naibu Waziri tumeyasikia wakati wote. Mradi wa mfereji anaousema wa DMDP ni mradi ambao tumeambiwa utatekelezwa tangu mwaka 2014 na wakazi wa kata zinazopitiwa na mradi huo waliambiwa wasiendeleze maeneo yao tangu 2014 wakiendelea kuhangaika na mafuriko kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna changamoto ya madaraja na barabara Kata ya Bonyokwa, Kata ya Kinyerezi, Kata ya Segerea, Kata ya Liwiti na kubwa kuliko ni Kata ya Tabata katika barabara ya kwenda Mwananchi, kalvati limebomoka na kwa sasa ninavyoongea…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali; je, ni lini mradi huo mkubwa wa DMDP utajengwa na barabara au Daraja la Kisiwani? Swali la kwanza.
Swali la pili, uanzishwaji wa TARURA umeondoa uwajibikaji wa Halmashauri sambamba na Madiwani moja kwa moja katika ujenzi wa barabara za mitaa. Je, Wizara ina mkakati gani kuhuisha kazi za TARURA ili waweze kutoa report katika Baraza la Madiwani ambalo moja kwa moja ndiyo wanawajibika kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kujua kero zao za moja kwa moja za barabara? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Theonest amesema imekuwa ni muda mrefu hadithi imekuwa ikisemwa, lakini utakubaliana nami kwamba katika majibu yangu kwenye swali la msingi, nimemwambia kwamba kandarasi tunatarajia itatangazwa mwezi Mei na mwezi Mei siyo mbali sana, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, tumeahidi tutatekeleza katika hili ambalo nimelisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameongelea juu ya suala zima la uanzishwaji wa chombo hiki cha TARURA na anachoomba ni namna gani TARURA watahuisha ili wananchi waweze kupata ushiriki wao kwa kupitia Waheshimiwa Madiwani na Wabunge?
Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ina wajibu wa kuhakikisha kwamba taarifa zake zinapelekwa DCC na DCC Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe, lakini Mwenyekiti au Meya ni Wajumbe na Wakurugenzi ni Wajumbe. Kwa hiyo, taarifa itakuwa inatolewa hapo na tutapata fursa ya kuweza kuwahoji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, pia kwenye chombo cha RCC ambapo sisi Waheshimiwa wote ni Wajumbe, naomba tushiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijaribu kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge kwamba kabla ya kuanzishwa kwa TARURA kila Mbunge na hasa kila Diwani alikuwa anaomba apate angalau hata kilomita moja ya kipande cha barabara au kalavati litengenezwe upande wake kiasi kwamba ule ufanisi (value for money) ilikuwa haionekani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tukienzi chombo hiki, bado ni mapema kabisa. Maeneo mengine ambayo TARURA imeanza kufanya kazi, wanapongeza. Naomba tukiunge mkono. (Makofi)
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri yanayotia moyo wananchi wa Jimbo la Chilonwa. Lakini pamoja na majibu mazuri sana naomba niwe na swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya sababu zinazofanya badhi ya watumishi kukwepa kwenda kufanya vijiji vya ndani ndani ni ukosefu wa nyumba za kuishi.
Je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kusaidia upatikanaji wa nyumba katika zahati zilizo vijiji vya ndani ndani sana? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwaka, Mbunge wa Ikulu kuwa kwanza naomba niipongeze Halmashauri ya Chilonwa kwa jinsi ambavyo wameweza kukamilisha zahanati nne. Yeye katika swali lake anauliza namna Serikali kuwezesha kupatikana nyumba za watumishi. Kama ambavyo amefanya kazi nzuri kwa kushirikiana na Halmashauri yao kuhakikisha wanakamilisha zahanati hizo ni vizuri jitihada hizo ambazo zimefanyika wakaanzisha uanzishaji na ukamilishaji wa nyumba za watumishi kwa sababu ni ukweli usiopingika kwamba ukiwa na zahanati nzuri bila watumishi kuwa na sehemu iliyo salama ya kwenda kufanyia kazi.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa mwenyekiti, ahsante, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba na mimi nimuulize Mheshimiwa Waziri.
Kwa kuwa wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Monduli katika Kata ya Makuyuni, Lemowoti na Halaramii wameonesha juhudi kubwa katika ujenzi wa vituo vya afya; na kwa kuwa Waziri wa TAMISEMI alivyokuja Monduli mwaka 2016 akiwa Naibu Waziri aliahidi kutoa michango kwa ajili ya kuunga mkono juhudi za wananchi wale. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ya kuwasiadia wananchi wale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri na kwamba na yeye mwenyewe atakiri na kuungana na jitihada za Serikali na hivi karibuni tumepeleka pesa katika vituo 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwamba safari ni hatua, azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba vituo vya afya vinajengwa katika kila kata. Kama tumefanya katika kata nyingine, naamini kabisa na kwake itakuwa katika safari ijayo.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pamoja na majibu ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, lakini naomba niwashukuru sana Serikali ya Korea, Serikali ya Tanzania na Manispaa ya Ilala ambayo inaongozwa na UKAWA na wananchi wa Kata ya Chanika kwa kutoa ushirikiano wa kupata hospitali kubwa ya mama na mtoto katika eneo hilo. Nashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwenye majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri anaonesha kwamba fedha kutoka Serikali Kuu ni shilingi bilioni moja, lakini kwenye bajeti ya TAMISEMI ambayo tumeshapitisha katika Bunge letu Tukufu ilionesha shilingi bilioni 1.5. Napenda nijue hii ni nyingine imeongezeka au ni ile ya shilingi bilioni 1.5 ambayo sasa imeshuka tena imekuwa one billion?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa kuna changamoto kubwa katika eneo hili na Mheshimiwa Waziri anakubali kwamba kuna mpango wa kujenga hospitali hii; je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kutembelea eneo hili aone kwanza eneo lipo vizuri, wananchi wametoa ushirikiano wa ekari 45 twende tufanye ziara ili waweke msukumo kwa kujengwa kwa haraka na kwa uhakika ili huduma ya afya iweze kupatikana katika eneo hili ambayo itahudumia Jimbo la Ukonga, Mkuranga na eneo la Kisarawe? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waitara anauliza kwamba katika orodha ya Hospitali za Wilaya 67 ambazo zinajengwa, kwa hesabu yake anaona ilikuwa inaonesha kwamba Hospitali ya Kivule imetengewa shilingi bilioni 1.5, lakini taarifa nilizonazo ni kwamba imetengwa shilingi bilioni moja kutoka Serikali Kuu, lakini ukiunganisha na shilingi bilioni mbili ambayo ni mapato ya ndani ya Manispaa, maana yake wao wanakuwa na shilingi bilioni tatu. Kwa ramani ambazo zinatolewa kwa ajili ya awamu ya kwanza ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya ni shilingi bilioni 1.5. Kwa hiyo, wao wako mara mbili yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwamba lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba hospitali zinajengwa za kisasa, lakini kwa kutumia utaratibu wa Force Account.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kiasi hicho ni cha kutosha tukisimamia tukahakikisha kwamba kila shilingi ambayo inatoka inaenda kufanya kazi iliyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili juu ya kwenda kutembelea maeneo hayo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nina mpango wa kwenda kutembelea eneo ambalo kinapanuliwa Kituo cha Afya cha Buguruni, Kinyerezi na maeneo mengine yote ili na mimi nijiridhishe tuwe katika page moja tunapoongea na Mheshimiwa Mbunge.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Njombe, Hospitali ya Kibena ndiyo hospitali inayotumika kama Hospitali ya Mkoa, lakini imechakaa sana na haina wodi ya wanaume wala x-ray.
Je, ni lini Serikali itatusaidia watu wa Njombe kupata wodi ya wanaume na x-ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala zima la kuchakaa Hospitali ya Wilaya ya Njombe ambayo kimsingi ilijengwa miaka ya zamani sana, tunakiri na tunatambua juu ya uchakavu huu. Kwa kadri bajeti itakavyoruhusu, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunazikarabati Hospitali za Wilaya ili zifanane na hadhi ya sasa hivi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, katika zile Hospitali ambazo zitakarabatiwa wakati bajeti ikiruhusu na Njombe nao hatutawasahau.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Moja, kwa kuwa kila penye mafanikio hapakosi kuwa na changamoto, je, Waziri sasa yuko tayari kufuatana na mimi kwenda Kituo cha Afya Mbwera kwenda kubaini baadhi ya changamoto za huu ujenzi unaoendelea hivi sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwamba hali ya Kituo cha Afya Kibiti majengo yake kwa kweli uchakavu wake hauridhishi. Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ya kufanya ukarabati Kituo hiki cha Afya Kibiti ili kiweze kutoa huduma yenye tija kwa wananchi wa Kibiti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ungando Mwenyekiti wa Wandengereko (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko tayari kwa sababu wanasema seeing is believing kama ambavyo juzi nilipata fursa ya kwenda Dar es Salaam kutembelea Kituo cha Afya Buguruni na kule inakojengwa Hospitali ya Wilaya kwa Mheshimiwa Waitara, niko tayari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kukarabati kituo kingine cha afya ambacho Mheshimiwa Mbunge anaomba, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba tunakamilisha na kukarabati vituo vya afya vingi kadri iwezekanavyo ili kusogeza huduma ya afya na hasa afya ya mama na mtoto kwa kadri itakavyowezekana. Kwa hiyo, kadri bajeti inavyoruhusu naomba nimhakikishie Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba ukarabati unafanyika.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kituo cha Afya Kakonko kimeelemewa sana na wagonjwa. Kituo hiki cha Afya Kakonko Waziri wa TAMISEMI akiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Jafo, aliwahi kukitembelea akaona ukubwa wa kazi inayofanyika katika kituo kile. Kinapata mgao wa dawa sawa na Kituo cha Afya, kinatoa huduma kama Hospitali ya Wilaya. Sasa ni lini Serikali kwa makusudi kabisa itajenga Hospitali ya Wilaya ya Kakonko ili kuondoa mzigo kwenye Kituo cha Afya cha Kakonko? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba maeneo yote ambayo kuna Vituo vya Afya na hakuna Hospitali za Wilaya, hivyo Vituo vya Afya ndivyo ambavyo vimekuwa huduma kama Hospitali za Wilaya. Ni ukweli usiopingika kwamba sifa ya kituo cha afya na sifa ya Hospitali ya Wilaya ni tofauti. Ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo hakuna Hospitali ya Wilaya tunajenga na ndio maana tumeanza na hizo hospitali 67. Ni azma kuhakikisha Wilaya zote Tanzania zinakuwa na Hospitali za Wilaya.
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Ulaya kinatumika kwa wananchi wote wa Kata za Zombo, Muhenda pamoja na Ulaya, lakini kina upungufu mkubwa sana wa watumishi na hali mbaya sana ya miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini Serikali itatupia macho kwenye Kituo cha Afya cha Ulaya ili wananchi wa pale kwenye Tarafa ya Ulaya waweze kupata tiba bora kwa mama na watoto, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE) Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya hicho Kituo cha Afya ambacho Mheshimiwa Mbunge anakitaja cha Ulaya sijapata fursa ya kukitembelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ni ukweli usiopingika kwamba miongoni mwa mikoa ambayo imepata Vituo vya Afya vya kutosha katika awamu hizi ni pamoja na Mkoa wa Morogoro pamoja na Hospitali ya Wilaya. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vyote ambavyo vinafanya kazi kama Vituo vya Afya, lakini havina hadhi ya Vituo vya Afya tunaenda kuvikarabati na kuviboresha ili vifanane na hadhi ya Vituo vya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni azma ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na yeye na pale alichombeza akaimba na wimbo nina amini hatutamsahau.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba uniruhusu niwape pole sana wenzetu wa Yanga kwa sababu msiba wa jirani yako ni msiba wa wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba asiwe na wasiwasi, naomba awe na subira mwaka 2018/2019 hii inakuja tutashughulikia suala lake la Ulaya.
MHE. BONIPHACE P. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ujenzi wa Vituo vya Afya katika nchi yetu kwa maeneo mbalimbali. Kuna vituo vimepata shilingi milioni 500 na kuna vituo vimepata shilingi milioni 400. Sasa huwa najiuliza na wanasema vituo vyote vimepata shilingi milioni 700; shilingi milioni 200 kwa vituo vilivyopata shilingi milioni 500 inaenda MSD na shilingi milioni 300 kwa vituo vilivyopata shilingi milioni 400 imeenda MSD. Sasa huwa najiuliza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tofauti ya fedha za kwenda kununua vifaa MSD ya shilingi milioni 300 na shilingi milioni 200 na shirika ni lile lile, la Serikali tofauti yake inatokana na nini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili linajirudia kwa mara nyingine na nikiwa hapa niliwahi kutoa ufafanuzi kwamba kwanza inategemeana na source of fund; kuna maeneo mbalimbali ambayo tumepata fedha.
Kwa hiyo, inategemea shilingi milioni 500 au shilingi milioni 400, kama ni Benki ya Dunia, Canada, Serikali ya Tanzania lakini pia inategemeana na hali ya Kituo cha Afya husika kwa sababu kuna baadhi ya Vituo vya Afya vinahitaji ukarabati mdogo, vingine ukarabati wake ni mkubwa. Kwa hiyo, tumekuwa tukifanya scope kujua uhalisia ili Kituo cha Afya kiweze kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala zima la pesa ambazo zinapelekwa MSD, majibu yake hayana tofauti sana na hili jibu la mwanzo kwa sababu ukienda Kituo cha Afya Manyamanyama ambacho labda kina x–ray center haiwezi kuwa sawa na kituo cha afya kingine ambacho hakina mashine kama hiyo.
Kwa hiyo, Serikali tumekuwa tukiyazingatia hayo wakati tunapeleka fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Korogwe hususan Korogwe Mjini tuna Hospitali ya Magunga, lakini tuna kata mbili ambazo zipo mbali nje ya mji kabisa, Kata ya Kwamsisi na Kata ya Mgombezi ambazo zina vijiji kama sita sita. Je, Serikali itakuwa tayari kutusaidia kupata fedha kwa ajili ya kuwajengea vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo imeelekezwa kwenye Ilani ya CCM kwamba Serikali ina wajibu wa kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya kila kata, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni suala tu la bajeti na safari ni hatua. Yeye mwenyewe ni shuhuda jinsi ambavyo tumeanza ujenzi wa vituo vya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kabisa wakati mwingine hatua nyingine itafika mahali ambapo hizo kata ambazo zipo mbali zitafikiwa kwa sababu ndiyo azma ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Sera ya Afya inazungumzia zahanati kwa kila kijiji, vituo vya afya kwa kila kata na hospitali za wilaya katika wilaya, jambo ambalo sera hii haijakamilika hasa katika Mkoa wetu wa Rukwa ambao hauna Hospitali ya Wilaya hata moja, ni lini sera hii itakamilika kikamilifu hasa katika Mkoa wetu wa Rukwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetoka kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mary Chatanda na Mheshimiwa Khenani ni shuhuda kwamba miongoni mwa Wilaya 67 ambazo zinaenda kujengewa Hospitali za Wilaya, ni pamoja na Wilaya ya Kalambo, Sumbawanga Vijijini pamoja na Wilaya ya Nkasi. Sasa siyo rahisi kusema lini exactly kwa sababu na ujenzi nao ni process, lakini na yeye mwenyewe ni shuhuda jinsi ambavyo Serikali imeazimia na inatekeleza.
MHE. RISALA S. KABONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nimesikia majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa idadi ya wagonjwa wanaotibiwa katika Hospitali ya Vwawa ni kubwa, out patient tu wanaotibiwa pale ni 150 mpaka 200 kwa siku. Je, Serikali kwa nini isijenge jengo kubwa la OPD ili kuweza kukidhi mahitaji ya wagonjwa wanaopata huduma kwa sasa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, idadi ya wanawake wanaojifungua katika Hospitali ya Vwawa ni kuanzia 15 mpaka 20 kwa siku, huku vifo vya watoto kuanzia sifuri mpaka miezi 28 ni 180 kwa takwimu za2015. Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kuongeza Madaktari, Wauguzi na vifaa tiba ili kupunguza vifo vya akina mama na watoto katika Hospitali ya Vwawa na pia kupunguza vifo vya wananchi katika Mkoa wetu wa Songwe? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la msingi la Mheshimiwa Risala aliongelea suala zima la kuwa na Hospitali ya Rufaa na katika majibu ambayo tumetoa tunamhakikishia na taratibu za ujenzi zimeshaanza na pesa imeshapelekwa. Sasa katika swali lake la nyongeza anarudi tena katika ile hospitali ambayo tumesema kwamba itaendelea kuwa Hospitali ya Wilaya na kwa sasa hivi inatumika temporarily kama Hospitali ya Rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge, ni vizuri tuchague njia moja ya kupita, hatuwezi kuwa na mawili kwa wakati mmoja. Jitihada ambazo zinafanyika na Serikali za kuhakikisha kwamba inajengwa Hospitali ya Rufaa ikizingatia ramani ya Hospitali ya Rufaa ni vizuri tukaiheshimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anaongelea juu ya suala zima la vifo vya watoto na akina mama kutokana na upungufu wa madaktari. Naomba nimhakikishie na yeye alikuwepo wakati Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Utumishi akiwa anatoa takwimu juu ya tarajio la Serikali la kupata vibali kwa ajili ya kuajiri watumishi wa sekta ya afya na elimu, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba tunaajiri watumishi wa kutosha ili kupunguza vifo vya mama na mtoto. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa uongozi wa Mkoa wa Arusha chini ya Mkuu wa Mkoa Ndugu Mrisho Gambo, anafanya jitihada mbalimbali za ujenzi wa vituo vya afya na zahanati katika Mkoa wetu wa Arusha. Mfano tu katika Jiji la Arusha kuna ujenzi wa Kituo kikubwa cha Afya cha Murieth pamoja na Hospitali ya Wilaya ya Arusha Mjini unaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kufahamu, Serikali imejipanga vipi kutuletea watumishi mara tu vituo hivi vitakapokamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba uniruhusu nichukue fursa hii kuupongeza Mkoa wa Arusha kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika suala zima la ujenzi wa vituo vya afya na hasa hicho Kituo cha Afya cha Murieth maana na mimi nimeenda kukitembelea, ni miongoni mwa Vituo vya Afya ambavyo vimejengwa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vinapokamilika huduma ziweze kutolewa na hakuna Kituo cha Afya hata kimoja ambacho kitakamilika Serikali ikakosa kupeleka watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie, immediately baada ya kwamba Vituo vya Afya vyote vya Arusha na maeneo mengine vikishakamilika, Serikali itapeleka watumishi pamoja na vifaa ili huduma za afya ziweze kutolewa kama ambavyo Serikali imekusudia. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nadhani waliomwandikia Mheshimiwa Naibu Waziri hawakunielewa vizuri. Swali langu nimeuliza hivi, ni kwa kiwango gani barabara za mitaa ina maana kutoka barabara ya Segerea kwenda Mandela road tutaweza kupunguza foleni. Kwa maana tutafungua vipi barabara za mtaa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameainisha kwamba wametenga fedha ya ujenzi wa barabara kutoka Barakuda
- Chang’ombe, sasa ukitoka Barakuda - Chang’ombe bado hawajapunguza foleni. Wangesema kutoka Barakuda - Chang’ombe - Kimanga ili wananchi wapite Kisiwani wasiingie Mandela road. Vivyo hivyo kutoka Kinyerezi - Kimara watu waingie Morogoro road wasirudi barabara ya Segerea, tuna changamoto sana ya foleni. Vivyo hivyo …
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali ni lini barabara ya Segerea itapunguziwa foleni kwa kuboresha barabara za mitaa zinazotoka na siyo kurudi barabara kwenye moja? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wamesema wametenga fedha kwa ujenzi wa daraja wa Tabata Kisiwani. Namwomba Naibu Waziri aje tumuonyesha daraja hilo kwa sababu lina changamoto kubwa. Matajiri wamevamia eneo, daraja haliwezekani kwa sababu mkondo ni mdogo. Ni lini atakuja kuona changamoto ili kuwaondoa wale watu tuweze kujenga daraja pale? Vinginevyo ni kupoteza fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimeeleza barabara ambazo zinatengenezwa na tafsiri yake ni nini? Mwananchi ambaye alikuwa anataka kwenda Segerea ana-option ya kutumia barabara ya zingine na ambacho kimekuwa kikitokea ni kwamba hizi barabara zikiwa mbovu sana hata ambaye angeweza kupita kwa Mnyamani hawezi kupita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kadri barabara hizi zingine zinavyotengenezwa inampa nafuu mwananchi wa maeneo hayo. Si kwamba gari zote ambazo zinazopita huko wanataka ni kwa sababu barabara za mtaani zinakuwa siyo nzuri. Aidha, kwa Jiji la Dar es Salaam kuna mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tunali-decongest, mpango uko vizuri, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira hilo liko mbioni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana na daraja ambalo analizungumzia na kuuliza nitakwenda lini, weekend iliyopita nilienda nikafika mpaka Mnyamani bahati mbaya tu Mheshimiwa Mbunge hakuwa na taarifa. Mimi niko tayari kwenda kwa kadri nafasi itakavyoruhusu ili tukatizame site kuona nini kilichopo ili tuweze kushauri vile ambavyo inatakiwa.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tatizo lililopo katika Jimbo la Segerea linafanana pia na lililopo katika Jimbo la Temeke ambapo katika Kata za Buza, Tandika na Kata 14 Temeke barabara zimeharibika sana na hasa baada ya mvua hizi. Kwa kuwa kata hizi hazipo katika ule mpango DMDP, nilitaka kujua Serikali ina mpango gani kwenda kukarabati barabara za mitaa katika kata hii angalau kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba baada ya mvua kunyesha maeneo mengi miundombinu yake imeharibika na hasa kwa Jiji la Dar es Salaam ambapo mvua zimenyesha nyingi sana.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya tathmini ya uharibifu uliotokea ili tujue hatua za dharura za kuchukua ili wananchi waendelee kutumia barabara katika hali nzuri.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, kupitia fedha ya Mfuko wa Barabara na fedha ya Benki ya Dunia mtandao wa barabara ya lami katika Manispaa ya Moshi unaridhisha kwa kiwango fulani, lakini kwa kuwa fedha hizi hazina mahusiano ya moja kwa moja na ahadi ya Rais ya kilometa 10 aliyoitoa siku tano kabla ya kufunga kampeni zake mwaka 2015. Je, Waziri haoni kwamba, kuna sababu ya kumkumbusha Rais huenda akawa na nafasi ya kukumbuka ile ahadi yake ya kilometa 10 katika Manispaa ya Moshi?
Mheshimiwa Spika, lakini la pili, tangu TARURA imeanza kazi Manispaa ya Moshi speed yake ya uwajibikaji haijaenda kwenye kasi ile ambayo Halmashauri ya Manispaa ya Moshi ilikuwa inafanya wakati inasimamia barabara zake.
Je, Waziri haoni kwamba, kuna haja ya kuisukuma TARURA ili iweze kuongeza kasi ili kuhakikisha kwamba, barabara ambazo zimeharibiwa sana na mvua kipindi hiki cha mvua zinakarabatiwa, ili ziwe katika hali nzuri kama ilivyokuwa wakati Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inasimamia yenyewe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anasema kwamba utekelezaji wa hizi barabara hauna uhusiano wa moja kwa moja na ahadi ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Spika, ni vizuri tu akatambua kwamba fedha zote ambazo zimefanya kazi ya ujenzi wa barabara katika Mji wa Moshi ni utekelezaji na mwenye fedha ni Mheshimiwa Rais yeye mwenyewe. Najua ana kiu, angependa barabara nyingi zaidi zijengwe, lakini haiondoi ukweli kwamba tumefanya kazi kubwa sana katika ujenzi wa barabara katika Manispaa ya Moshi.
Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili, anasema haridhishwi na kasi ya chombo hiki ambacho tumeanzisha, TARURA, ukilinganisha na hapo awali jinsi ambavyo wao halmashauri walikuwa wakifanya.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie, chombo hiki ni baada ya kilio cha Waheshimiwa Wabunge wengi ambao tulikuwa tunapenda barabara zetu zichukuliwe na TANROADS, TARURA katika maeneo mengi inafanya kazi vizuri na Moshi naamini nao watafanya kazi vizuri. Hebu tukilee na tuhakikishe kwamba tunakisukuma tunakipa nguvu kifanye kazi iliyotarajiwa. (Makofi)
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Halmashauri tano za Mkoa wa Dodoma zilipata fedha za kujenga barabara za mijini, lakini halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa na Kongwa hatukupata na nimezungumza na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kongwa kwamba Mpwapwa na Kongwa hatukupata barabara za kujenga mjini na ilikuwa ni ahadi ya Waziri wa TAMISEMI, tarehe 30 Desemba, Mheshimiwa Jafo.
Naomba maelezo ya Waziri kwa nini, Kongwa na Mpwapwa hatukupata hizi hela katika hiyo bajeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yale yote na hasa kwa sababu na yeye amesema kwamba ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri, naomba nimhakikishie dhamira ya dhati ipo, lakini ni ukweli usiopingika kwamba miji mingine yote kwa Mkoa wa Dodoma imepata. Maana yake katika hatua inayofuata lazima tuhakikishe kwamba na maeneo hayo mawili ikiwepo eneo la kwako Mheshimiwa Spika yanatiliwa mkazo, ili barabara zijengwe kwa kiwango cha lami na kwa Mheshimiwa Lubeleje. Naomba nilichukue kwa mikono miwili kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba, na hasa kwa kuanzia kwa Mheshimiwa Spika hatukusahau hata kidogo. (Makofi)
MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Masasi imeandika andiko hilo TEA katika kipindi cha takriban miaka miwili iliyopita na mpaka sasa hakuna majibu yoyote au matumaini yoyote ya kupatikana kwa fedha, je, ni lini sasa Serikali kupitaia TEA itatoa fedha hizo ili kuboresha miundombinu ya shule hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tangu tulipoambiwa Serikali ina mpango wa kuajiri Walimu 5,000 ni muda sasa umepita, lini sasa Serikali itatoa kauli ya kuajiri Walimu hao rasmi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Rashid Mohamed Chuachua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza anauliza juu ya Halmashauri kupeleka maombi TEA na kwamba mpaka sasa hivi bado majibu hayajaja kwa ajili ya upatikanaji wa fedha na miundombinu iweze kuboreshwa ili Form Five na Six zianze kufanya kazi katika Halmashauri ya Masasi. Ni ukweli usiopingika kwamba ili tuweze kuchukua vijana wa Form Five na Form Six ni lazima miundombinu ambayo inatakiwa iwe imakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Halmashauri yake, hivi karibuni Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliwaita Wakurugenzi wote pamoja na Wenyeviti ili waweze kuweka vipaumbele katika maeneo ambayo wanaenda kuboresha katika suala zima la elimu na afya. Ni matumaini yangu makubwa kwamba pamoja na ombi ambalo limepelekwa TEA kwa vile priority yao ni suala la elimu watakuwa wameweka kama kipaumbele ili tuweze kukamilisha miundombinu ya shule hizo mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala zima la kuajiri Walimu, bahati nzuri Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana wakati anahitimisha bajeti yake alisema hapa nasi sote tukiwa mashuhuda. Naomba Mheshimiwa Mbunge awe na imani kama ambavyo tulisema kwamba vibali vitapatikana kwa ajili ya watumishi wa afya na tayari kazi zilishatangazwa, hatua itakayofuata ni hao Walimu ambao Serikali imeahidi kuajiri.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Changamoto ya Walimu wa Sayansi iliyoko Masasi pia inaukumba Mkoa wangu wa Iringa. Nataka commitment ya Mheshimiwa Waziri kwamba watakapopewa vibali vya kuajiri Walimu wa Sayansi mtaupa kipaumbele Mkoa wa Iringa? Nilitoa mfano last time kuwa Shule ya Lukosi ina watoto 700 na tuna Mwalimu mmoja tu wa Sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rose Tweve, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yale yote ambayo yana upungufu mkubwa wa Walimu wa Sayansi ndiyo hayo ambayo hasa yanaanza kupelekewa Walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niutake Mkoa wa Iringa kwa ujumla wake watupe stock, maeneo ambayo yana upungufu mkubwa hayo ndiyo yawe ya kwanza katika kuhakikisha kwamba walimu wanapelekwa kwa ajili ya kwenda kuziba pengo hilo. Naamini na Iringa nao watafanya hivyo.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa maswali ya Shule za Sekondari za Wasichana katika eneo la Masasi linafanana kabisa na Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Mpanda iliyoko Mpanda Mjini na tumeshaleta maoni kwa Waziri wa Elimu pamoja na Waziri wa TAMISEMI kwamba shule ile ilikuwa inachukua kuanzia Form One mpaka Form Four na ikabadilishwa ikawa Form Five mpaka Form Six. Je, ni lini sasa Serikali itakuja na mpango wa kuhakikisha shule ile inachukua wasichana kuanzia Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita kwa kuwa tuna shule moja tu Mkoa wa Katavi ya boarding? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pudenciana Kikwembe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Kikwembe kwa sababu ni miongoni mwa Wabunge wachache ambao huwa wakiwa katika maeneo yao ya Jimbo ambao ni Walimu huwa wanaenda kushika chaki kwa ajili ya kusaidia watoto wetu. Naye ni Mwalimu mzuri wa masomo ya Sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika swali langu la msingi kwamba ni wajibu kuhakikisha kwamba miundombinu yote inayohusika katika uanzishaji wa ‘A’ Level inakamilika, lakini pia ithibati iweze kupatikana na Kamishna wa Elimu aweze kutoa kibali, hapo ndipo tunaposajili shule yetu kwa ajili ya kuanzisha Form Five. Kwa hiyo, naamini na shule anayoitaja Mheshimiwa Mbunge, pindi miundombinu itakavyokuwa imekamilika, Serikali haitasita kwa sababu uhitaji wa ‘A’ Level ni suala ambalo hatuna ubishi katika hilo.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naishukuru sana Serikali kwa kuendelea kujenga barabara za lami kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais. Naomba sasa nimwulize Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Igunga imekuwa ikisuasua kwa miaka minne sasa kuilea hii Mamlaka ya Miji Mdogo; na kwa kuwa Mkurugenzi mara kadhaa amesikika akisema kwamba hii Mamlaka ya Mji Mdogo inaweza kufutwa wakati wowote, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuwaita Mkurugenzi, Mwenyekiti wa Halmashauri na Mtendaji wa Mamlaka hiyo ili waje hapa wapate maelekezo maalum ili waweze kuilea vizuri kama sheria inavyosema?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa idadi ya wakazi wa Mji wa Igunga sasa imezidi, wako zaidi ya 50,000 kiwango ambacho kinaruhusu kuanzishwa kwa mamlaka kamili; na kwa kuwa makusanyo ya mapato kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Igunga pale mjini sasa hivi yanaweza kuzidi shilingi bilioni 2, kiasi ambacho kinaweza kuiendesha mamlaka kamili. Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuanzisha Mamlaka Kamili ya Mji wa Igunga?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Dalaly Kafumu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala zima la kumwita Mkurugenzi pamoja na Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hata kabla ya kuwaita, katika maeneo ambayo tulitakiwa kutembelea, nami mwenyewe binafsi nilitakiwa kutembelea ni pamoja na Igunga. Naomba nimhakikishie, kuna mambo mengine ambayo tutajadiliana tukiwa site, naamini naye Mheshimiwa Mbunge akiwepo, ili kwa ujumla wake tulitazame suala hili tuone namna nzuri ya kuhakikisha kwamba Halmashauri inaendelea kuwa na nguvu yake lakini na Mji Mdogo nao uendelee, kwa sababu lengo ni kuhakikisha kwamba Igunga inaendelea kwa kasi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili ambalo ameuliza kwamba kwa kiasi ambacho pesa inakusanywa na Mji wa Igunga, ifike mahali ambapo sasa iweze kujitegemea kwa kuwa na mamlaka kamili, ni jambo jema. Hata hivyo, nayo ina tafsiri yale tofauti. Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba Halmashauri ya Igunga inakuwepo pamoja na vyanzo vyake kwa ujumla. Sasa kuna uwezekano mkubwa ambapo ukisema Halmashauri ya Mji ijitenge, maana yake Halmashauri nayo inategemea vyanzo kutokana na mji, ikiunganisha na vile ambavyo ni vya nje ya mji ndiyo maana Halmashauri ya Igunga inakuwepo. Kwa hiyo, ni vizuri suala hili kwa picha kubwa zaidi ili tuone namna nzuri kutoiua Halmashauri ya Igunga lakini wakati huo huo Mamlaka ya Mji Mdogo wa Igunga nayo ifanye kazi kama ilivyokusudiwa na wananchi.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyo Mji Mdogo wa Igunga, Mji wa Katesh nao ulianzishwa kuwa Mamlaka Ndogo ya Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, lakini ni kweli kwamba Halmashauri haiipi kipaumbele hii Miji Midogo iliyoanzishwa. Je, Serikali itaweka utaratibu mzuri wa kuona hii Miji Midogo iliyoanzishwa inapata hela au kuipandisha hadhi? Kama sivyo, miji hiyo itabaki inadumaa na wakati ndiyo inayotoa mapato makubwa kwa Halmashauri. Naomba Serikali iseme wataweka utaratibu huo lini ili Miji Midogo iwe na uhakika wa kuendelea? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo nia ya Serikali kukiuka kile ambacho kinaitwa D by D. Kwa mujibu wa Katiba ni sisi ambao tuliamua kwamba tunapeleka madaraka kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kwa kupitia vikao vyetu ambavyo naye ni Diwani anaporudi kule, sisi tukiwa Madiwani kule ndiyo ambao tunafanya maamuzi kuona namna iliyo bora ya kuhakikisha kwamba Halmshauri zetu zinafanya kazi iliyokusudiwa. Itakuwa siyo busara Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwenda kuziingilia zile Halmashauri ambazo Waheshimiwa Madiwani wakikaa wana maamuzi ambayo ni sahihi nasi tunakuja kubariki kutokana na vikao vyao ambavyo ni halali.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora imetenga shilingi milioni 70 kwa ajili ya kuendeleza jengo la OPD; na kwa kuwa pesa hizo huenda zisikidhi kukamilisha jengo hili, je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha inawaongezea fedha Wilaya ya Tabora ili waweze kupata Hospitali ya Rufaa ili kuepuka wagonjwa kupelekwa Hospital ya Bugando au Muhimbili? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bafadhili, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Tabora tayari tunayo Hospitali ya Rufaa. Katika swali la msingi ambacho kinaulizwa ni Hospitali ya Wilaya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha Wilaya zote ambazo hatuna Hospital za Wilaya zinajengwa. Ndiyo maana tumeanza na hospitali 67. Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba fedha ambayo inapelekwa inaenda kutumika vile ilivyokusudiwa. Naomba nimkikishie, kama hicho kiasi cha fedha kilichotengwa shilingi milioni 70 hazitakidhi, Serikali itakuwa tayari kuhakikisha kwamba inaongeza fedha ili Hospitali ya Wilaya iweze kukamilika.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa baadhi ya Vituo vya Afya vimepewa shilingi milioni 500 ili vikamilishe ujenzi wake; na kwa kuwa ujenzi wa Kituo cha Afya Mbori, Wilayani Mpwapwa sasa ni miaka 10 haujakamilika. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutoa shilingi milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Afya Mbori ili waweze kukamilisha ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lubeleje, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi, ni azma ya Serikali kuhakikisha Vituo vya Afya 513 vinafanyiwa ukarabati ili ziweze kutoa huduma tunayokusudia. Namwomba Mheshimiwa Mbunge aridhike na kasi ya Serikali kwamba tumeanza na vituo 208 na juzi vimeongezeka viwili ikiwa ni Kituo cha Afya cha Kibondo na kingine Nsimbo. Baada ya wafadhili kuona kasi nzuri ya Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli kuhusiana na suala zima la afya, nao wameamua kuweka nguvu katika maeneo ambayo yanahudumia wakimbizi. Kwa hiyo, badala ya vituo 208 sasa tuna vituo 210.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa vikundi vingi vimehamasika na wengi wanahitaji mkopo na uwezo wa Halmashauri yetu siyo mkubwa kiasi hicho na katika Wizara mbalimbali tunazo fedha kwa ajili ya maendeleo ya vijana katika mifuko mbalimbali.
Ni lini TAMISEMI itaunganisha nguvu na Wizara nyingine ili sasa na sisi kule fedha hizo ziweze kuwafikia? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kila siku tunasikia kwenye vitabu vya CAG na Wabunge wakilalamika kwamba hizi fedha haziendi kwa wananchi kutoka kwenye halmashauri. Nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba sheria hii ya asilimia kumi kwenda kwa akina mama, vijana na walemavu itatekelezwa kiufasaha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la kwanza juu ya uwezo mdogo wa Halmashauri na kuitaka Serikali kuunganisha nguvu kupitia fursa tofauti tofauti, naomba nimhakikishie kama ambavyo amesema yeye mwenyewe kuna fursa kwa mikopo kwa vijana kupitia ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Uratibu ambayo iko chini ya Mheshimiwa Mhagama ni fursa ambayo ni vizuri wananchi wa Buhigwe wakaitumia katika kuweza ku-access mikopo.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili juu ya halmashauri kusuasua katika kutenga asilimia 10, anataka kauli ya Serikali. Kama ambavyo nimekuwa nikisema na leo narudia hata kama ingepatikana shilingi moja kinachotakiwa ni asilimia kumi ya shilingi moja hiyo itengwe. Kama ambavyo nilishawahi kujibu hapa katika moja ya maswali wakati tunaenda kukamilisha Finance Bill kuna kipengele ambacho kitampa Waziri mwenye dhamana ili iwe ni takwa la kisheria na kama kuna Mkurugenzi yeyote atashindwa kutenga fungu hilo hatua ziweze kuchukuliwa.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maelekezo yako lakini kipekee nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri japo ni marefu kama ambavyo umesema.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu hayo mazuri, naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, wananchi wa Halmashauri na Jimbo la Msalala kama walivyo ndugu zao wa Jimbo la Nyang’hwale na kwa kushirikiana na Mbunge wao hivyo hivyo nao wamefanya kazi kubwa sana ya kuanza kujenga shule mpya za sekondari, Shule za Mwazimba na Nundu ambazo miundombinu aliyoitaja Mheshimiwa Naibu Waziri karibia yote imekamilika, lakini shule hizi hazijapata kibali cha kufunguliwa.
Mheshimiwa Spika, nilitaka kujua ni lini shule hizi mbili za Nundu na Mwazimba katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala zitafunguliwa kuanza kupokea wanafunzi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Msalala kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo Msalala katika kipindi cha miaka minne iliyopita wamefanikiwa kujenga hosteli kwenye shule saba za sekondari za Kata, shule za Busangi, Baloha, Segese, Lubuya, Bulige, Ntobo…
Mheshimiwa Spika, samahani, naomba nimalizie tu swali langu fupi kwamba shule hizi zina watoto lakini hazitambuliwi na Serikali na hazipati ruzuku ya uendeshaji wa hosteli. Ni lini shule hizi zitatambuliwa na Serikali ili ziwe zinapata ruzuku ya gharama za uendeshaji wa hosteli hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge taratibu zifuatwe ili hizo shule ziweze kufunguliwa. Kwa sababu ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba pale ambapo miundombinu ya shule imekamilika zinaweza kufunguliwa ili wananchi wetu wapate huduma kwa karibu.
Mheshimiwa Spika, katika hilo la pili amesema kwamba hosteli zimejengwa sasa anataka Serikali ianze kuhudumia hosteli.
Mheshimiwa Spika, sina uhakika kama msingi wa swali ni juu ya kwamba hosteli ikishajengwa ianze kupata huduma, lakini kama nimemuelewa sawasawa kwamba anachomaanisha ni kwamba shule hiyo itambuliwe kwamba ni miongoni mwa shule za boarding, naomba tu tufuate taratibu ili wananchi na hasa vijana wetu ambao wana adha ya kutembea umbali mrefu hosteli pale inapokamilika huduma ziweze kutolewa.
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ni lini Serikali itawajengea nyumba walimu wale ambao hawana nyumba kabisa katika shule zao? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa mambo mazuri yanaigwa, je, Wakuu wa Mikoa hawaoni kama ni vizuri kumuiga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa Makonda nao waweze kutafuta wafadhili wa kuweza kuwajengea walimu nyumba za kuishi na ofisi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la upungufu wa nyumba za walimu, naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge kwamba katika hizo pesa ambazo zimeletwa za EP4R ni wajibu wa halmashauri husika kuangalia kama hitaji kubwa ni nyumba za walimu, hakuna dhambi pesa hizo zikatumika pia katika kuhakikisha nyumba zinajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, naamini ni wazo jema, naomba niwasihi Wakuu wa Mikoa mingine waige mfano mzuri kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge yeye mwenyewe ameliona na anapongeza juhudi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa Serikali imekiri kwamba mgogoro upo katika eneo hili, je, haioni haja ya kuharakisha kufuta eneo hili ili wananchi wale wapate maeneo ya kulima?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wananchi wale wana mahitaji makubwa ya ardhi, Serikali haioni haja sasa kupitia mipaka ya eneo lile ili kuongeza eneo la kijiji?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mpakate, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika swali langu la msingi atakubaliana na mimi kwamba hukumu ndiyo imepatikana Februari, 2018 na bado kuna tetesi kwamba huyu ambaye ameshindwa ni kama vile tayari ametuma application kwa ajili ya kukata rufaa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wale ambao wanahitaji eneo wanapatiwa lakini kwa kufuata sheria. Naomba tuvute subira taratibu zote zifuatwe ili wananchi wapate haki lakini na yule mwingine ambaye alikuwa anamiliki asije akasema kwamba haki yake imeporwa.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wakati wananchi wa Mkwaya hawajajua mmiliki halali wa eneo hili ni nani kwa kuwa kulikuwa na mgogoro baina ya Serikali na mwekezaji, wakati fulani Machi, 2017 wananchi waliamua…
Ahsante. Kuna watu wameshtakiwa wakati wanaomba hili eneo liweze kuchukuliwa na bado kesi ziko mahakamani lakini Serikali imeshinda kesi. Sasa Mheshimiwa Waziri, anasemaje kuhusu hawa watu walioshtakiwa wakati wanalipigania eneo hili? Ni hatua gani Serikali itachukua ili kuwasaidia wale watu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bobali, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anajua historia ya mgogoro huu kwamba inaanzia miaka ya 1995 na kwamba kuna wakati ambapo wananchi walivamia maeneo yale ya mwekezaji wakachukua ndizi na wengine wakaenda kutikisa mikorosho. Kwa hiyo, haiwezekani tukasema kwamba sasa hao ambao walivunja sheria Serikali iwatetee, ni vizuri sheria ikafuata mkondo wake.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa mahitaji ni walimu 17, kwa sasa wapo walimu 7, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha ikama ya walimu inakamilika katika Shule ya Msingi Kipela? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, watumishi wasio walimu wapo 7, mahitaji ya shule ile ni watumishi 13. Je, Serikali haioni wakati sasa umefika wa kuhakikisha idadi ya watumishi wasio walimu inakamilika kutokana na uhitaji wa shule? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zainabu Mwamwindi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu nimpongeze Mheshimiwa Mwamwindi kwa jinsi ambavyo amekuwa akiwapigania wananchi wake wa Mkoa wa Iringa katika kuhakikisha kwamba wanapata huduma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kutaka kujua Serikali ina mkakati gani, kwanza naomba nitumie fursa hii kuagiza Wakurugenzi wote kwa sababu umeshatoka Waraka kutoka Ofisi ya Rai, TAMISEMI ukiwataka Wakurugenzi wahakikishe kwamba wale walimu ambao wamejifunza elimu maalum wanapelekwa kufundisha katika shule maalum kwa sababu wana ujuzi nao. Kwa hiyo, ndani ya Mkoa wa Iringa na maeneo jirani ni vizuri Wakurugenzi wakahakikisha stock inachukuliwa ili wale walimu wote ambao wana ujuzi maalum waweze kupelekwa kabla huo mkakati wa pili wa ajira haujatekelezwa kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na upungufu wa watumishi ambao siyo wa taaluma ya elimu, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanapatikana kwa mujibu wa ikama lakini pia itategemea bajeti itakavyoruhusu.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kumekuwa na shida ya walimu wa alama kwa ajili ya wanafunzi viziwi. Je, Serikali inatoa commitment gani kuhakikisha tunapata walimu zaidi kuweza kuwasaidia watu wanaotumia alama katika kujifunza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi hawa walimu ambao wanatumia alama nayo ni elimu maalum. Kwa hiyo, sisi tunalitazama kwa mapana yake yote na ndiyo maana nimesema kwamba katika hao walimu watakaoajiriwa, naamini na hao wanaotumia alama ni miongoni mwa hao wenye uhitaji maalum na watachukuliwa ili kuweza kuhudumia wanafunzi wanaohitaji walimu wenye kutumia alama.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa hospitali hii inahudumia wagonjwa wengi kutoka Mkoa wa Mbeya, Singida na Tabora lakini ina Madaktari Bingwa wachache; Madaktari Bingwa waliopo ni wanne tu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha hospitali hii inakuwa na Madaktari Bingwa wa kutosha ili kutoa huduma bora kwa wakati wote?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa gharama za hospitali hii ya Mission pamoja na gharama nyingine za hospitali za binafsi ni kubwa sana ambapo wananchi wa kawaida hawawezi kumudu. Kwa mfano, mama anapoenda kujifungua anatakiwa kulipa Sh.150,000 kwa kawaida lakini anapojifungua kwa operesheni anatakiwa kulipa Sh.450,000. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Wilaya ya Itigi inapata Hospitali ya Wilaya? Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala zima la kuwepo Madaktari Bingwa wa kutosha, ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba wanapatikana ili waweze kutoa huduma. Hivi karibuni Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeweza kutoa tangazo kwa ajili ya Madaktari. Naamini katika wale ambao watakuwa wameomba na Madaktari Bingwa watapatikana kwa ajili ya kuwapeleka maeneo kama hayo.
Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira na swali hili limekuwa likiulizwa mara kwa mara na Wabunge wa Mkoa wa Singida, mnamo tarehe 7 mwezi huu swali hili liliulizwa na leo linaulizwa kwa mara ya pili. Kwa hiyo, inaonyesha jinsi ambavyo wanajali wananchi wao katika suala zima la afya.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na gharama za matibabu ambazo zinatolewa na hospitali hii na hospitali zingine binafsi, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi tunatarajia mwongozo kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa sababu Serikali inawekeza pesa zake, kuwe na bei ambazo wananchi wanaweza kumudu.
Mheshimiwa Spika, amechomekea na swali lingine kuhusiana na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Itigi, naomba nimhakikishie ni azma ya Serikali baada ya kuwa tumemaliza hizi hospitali 67, katika maeneo yote ambayo hakuna Hospitali za Wilaya Serikali itaenda kujenga.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nakubali kwamba Serikali inajitahidi sana kusaidia Hospitali ya Wilaya ya Urambo lakini bado tuna changamoto kubwa ambayo ni ukosefu wa theater, ni mradi wa ADB ambao ulijenga theater pale ikafikia lenta. Je, Serikali inawaliwaza vipi wapiga kura wangu wa Urambo kuhusu kumalizika kwa theatre ambayo ipo katika hatua ya lenta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nilipata nafasi ya kutembelea Urambo na naomba nimpongeze kwa dhati kabisa Mheshimiwa Sitta amekuwa ni mpiganaji kuhakikisha kwamba afya ya akinamama na watoto kwa ujumla inaboreshwa. Wakafanya kazi nzuri sana, wameanzisha na wodi maalum kwa wale watu ambao wangependa wawe kwenye grade A, ni jambo la kupongezwa na wengine ni vizuri tukaiga. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimeona ile theater ambayo inajengwa ikafikia usawa wa lenta, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Sitta Serikali itahakikisha kwamba kazi nzuri ambayo imefanyika haiachwi ikapotea, kwa kadri pesa itakavyopatikana tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba tunamalizia ile theater ambayo ilikuwa imekusudiwa kwa ajili ya kutoa huduma kwa akinamama na watoto. (Makofi)
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na mimi kupata swali la nyongeza. Ni wiki mbili zimepita alikuja Katibu wa Hospitali ya Mwambani Bwana Kalindu na nikamwita Mheshimiwa Naibu Waziri tukakaa, tukaongelea habari ya Hospitali ya Mwambani pale Mkwajuni.
Mheshimiwa Spika, kama mnavyojua Songwe ni Wilaya mpya na hatuna Hospitali ya Wilaya lakini hii Hospitali ya Mwambani ndiyo inayotumika kama Hospitali ya Wilaya au Hospitali Teule, lakini watumishi mpaka sasa ni haba na hatupati dawa na hata mgao wa Serikali hauendi kama ambavyo inatakiwa ipewe Hospitali Teule. Ni nini Serikali inatamka juu ya jambo hili na Mheshimiwa Waziri anajua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Mulugo alikuja na tukakaa pamoja na Daktari ambaye alikuwa ametoka Hospitali ya Mwambani. Kimsingi Hospitali ya Mwambani kwa sababu ndiyo hospitali pekee iliyopo inatakiwa itumike kama DDH. Ni makosa tu ambayo yalifanyika na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ndani ya muda mfupi tatizo litakuwa limeshatatuliwa na hospitali ile itatambuliwa kama DDH kwa sababu ndiyo hospitali ambayo ni tegemeo kwa wananchi wa Mwambani na Chunya kwa ujumla wake. (Makofi)
MHE. OMARY A. BADWEL: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza kwa kuwa Serikali imeunda chombo kinaitwa TARURA na wakati huo kabla ya kuunda TARURA barabara zilizokuwa zinahudumiwa na Halmashauri ikaonekana utekelezaji wake si bora. Kwa kuwa tayari Serikali imeunda chombo hiki TARURA na lengo lake lilikuwa ni kuzifanya hizi barabara za mijini na vijijini kufikia hadhi kama hii ambayo tunaiomba kupandishwa hadhi kwa barabara. Je, nataka kujua bado kuna haja ya kuendelea kuomba kupandishwa hadhi barabara zetu au TARARU ielekezwe kuchukua nafasi ya kutengeneza barabara hizi vizuri kama ilivyokuwa inatengeneza TANROADS? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali imeunda chombo hiki kwa ajili ya kuboresha hizi barabara lakini bado kuna tofauti ya TARURA na TANROADS kwa maana ya asilimia ya fedha wanazopewa na Serikali ambapo TANROADS wanapata asilimia 70 na TARURA wanapata asilimia 30. Je, ni lini sasa Serikali itazigawia sawa kwa sawa taasisi hizi mbili kwa maana ya TARURA wapate asilimia 50 na TANROADS wapate asilimia 50 ili utengenezaji wa barabara hizi uwe katika kiwango kinachokusudiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Badwel, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na kilio cha Waheshimiwa Wabunge kutaka barabara zao zipandishwe hadhi ili ziweze kuhudumiwa na TANROAD. Pia ni ukweli usiopingika kwamba tangu tumeanzisha chombo hiki cha TARURA ambacho kimsingi kinafanya kazi nzuri, kuna umuhimu wa kutathmini kama iko haja ya kutaka kupandishwa tena barabara hizi. Naamini kinachotakiwa ni kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa kwa viwango ili zilingane na zile ambazo zinazojengwa na TANROADS.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kuhusu mgawanyo, iko haja lakini ni vizuri pia tukazingatia kwamba barabara nyingi ambazo zinajengwa na TANROADS zinajengwa kwa kiwango cha lami na barabara ambazo zinazojengwa kwa kiwango cha lami zinauhitaji mkubwa wa fedha ukilinganishwa na ambazo nyingi zinajengwa kwa changarawe na udongo. Kwa hiyo, ukifika wakati ambapo haja ikawepo kwamba tugawanye 50 kwa 50, naamini kwa mujibu wa taratibu zitakazofuatwa na Bunge lako likiidhinisha kwa mujibu wa sheria tutafika huko kwa siku za usoni.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza naishukuru Serikali kwa kufanya tathimini ya ujenzi wa madaraja haya. Eneo hili ni muhimu sana kwa uzalishaji wa zao la korosho na wananchi wanapata shida kweli wakati wa kusafirisha korosho kupeleka mnadani. Sasa je, Serikali leo inatoa tamko gani kwamba ni lini ujenzi huu unaanza hata kama ni kwa awamu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kikwazo kikubwa cha ujenzi huu ni bajeti ndogo ambayo wamepewa TARURA. Sasa je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha ambazo zinaenda TARURA ili ujenzi wa madaraja nchini uweze kwenda kwa kasi inayotakiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavo nimekiri kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba umuhimu wa madaraja haya haina ubishani; lakini pia ni ukweli usiopingika kwamba ili kujenga madaraja haya kwa kiasi cha pesa kama tulivyotaja kwenye tathmini, bilioni 3.5 ni kiasi kingi cha fedha. Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge aiamini Serikali kwamba ina nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba changamoto hii inatatuliwa ipo kinachogomba ni bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anauliza uwezekano wa TARURA kuongezewa fedha ili iweze kufanya kazi kubwa. Jana nilijibu swali la nyongeza, kwamba ni vizuri pia tukazingatia kazi kubwa ambayo inafanywa na TANROADS na TARURA ndiyo tumeanza kuijenga, tuipe muda tuone namna ambavyo inatenda kazi kwa sababu pia itakuwa si busara kusema kiasi kingi cha fedha kitoke TANROADS kiende TARURA kwa sababu nao wana kazi kubwa ya kujenga barabara kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ukweli utabaki pale pale kwamba TARURA inahitaji nyongeza ya fedha. Pamoja na ubovu wa daraja liko tatizo la barabara ambazo zina mawe hazipitiki, kwa mfano katika Jimbo la Rombo, Kata za Handeni, Shimbi, na Makiidi ni Kata ambazo zilikumbwa na volkano na kwa hiyo mawe ni mengi barabara hazitengenezeki. Sasa, je, ni mkakati gani Serikali itakayofanya ili barabara kama hizi ziweze kupitika kwa sababu Vijijini ndiko kwenye uzalishaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na yeye kwamba kuna baadhi ya ameneo ambayo uhitaji wa pesa ni mkubwa. Kwa hiyo iko case by case, naomba Mheshimiwa nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI imekuwa ikichukua case by case, pale ambapo kuna uhitaji maalum kuna fedha ambazo zimekuwa zikitengwa ili kutatua changamoto ambazo zinakuwa zinawakabili wananchi wa maeneo husika.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa daraja la Gwedegwede lilisombwa na maji wakati wa masika; na kwa kuwa wananchi wa Kata wa Zagaligali, Mbuga, Lumuma, Pwaga na Godegode wanazunguka mpaka Kibakwe, zaidi ya kilomita 75 ndipo wafike Mpwapwa Mjini. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga daraja la Godegode ili kuondoa usumbufu kwa wananchi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja ambalo Mheshimiwa analitaja ana uelewa mzuri na daraja hilo. Naomba baada ya kumaliza kipindi hiki cha Bunge tuwasiliane ili tujue; kabla ya kuanza kujenga daraja hilo lazima tufanye tathimini tujue gharama kiasi gani cha fedha inahitajika ili tuhakikishe kwamba daraja hilo linajengwa ili kuondoa adha kwa wananchi ambao wanalazimika kuzunguka umbali mrefu.
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na pia nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa suala la madaraja yanayounganisha Wilaya kwa Wilaya au hata Kata kwa Kata ni ya muhimu sana; Ileje tulijiongeza kuhusiana na suala hilo kuwa fedha inayohitajika ni kubwa, lakini mahitaji yaliyopo ni madogo. Kwa hiyo tumeomba kwa ombi maalum kuomba fedha ya kimkakati kwa ajili ya daraja linalopita mto Mwalwisi ambalo ndiyo linalotumika na mgodi wa makaa ya mawe Kiwira na Kabulo. Kwa hiyo nilitaka kujua hatima yake ni nini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kutembelea Ileje, na nimefika Jimboni kwake naomba nimpongeze sana jinsi ambavyo wananchi wa Ileje; hakika Ileje ambayo ilikuwa inatazamwa miaka hiyo siyo Ileje ya sasa hivi, Ileje inafunguka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba katika maeneo ambayo yana uwekezaji wa kimkakati ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba yanatatuliwa changamoto ili tunapoongelea kwenda kufuata makaa ya mawe kule isiwe ni adha. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika mipango ya Serikali ya kuhakikisha kwamba makaa yale tunaanza kuyatumia lazima tufike daraja likiwa limekamilika. (Makofi)
MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa barabara ya Nzasa – Kilungule – Kwa Mwanagati na Buza ni muhimu sana kwa wakazi wa Mbagala, kwa maana ya Jimbo la Temeke na vile vile kwa wakazi wa Jimbo la Ukonga. Je Serikali, ina mpango gani wa muda mfupi wa kuweza kuboresha barabara hiyo ili wakazi hao waweze kupita kwa ufasaha na wepesi kusafirisha mazao na huduma za kijamii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Wilaya Kisarawe, imepakana na Mkoa wa Dar es Salam na Jimbo la Ukonga; na kwa kuwa barabara inayopita Msimbu inaanzia Chanika. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha au kujenga lami ya muda mrefu barabara inayoanzia Chanika – Msimbu hadi Masaki ambapo itaungana na barabara ya Mwanaromango ili kusaidia ujenzi wa taifa na kuendana na speed ya Mheshimiwa Rais kwa sababu tuko kwenye awamu ya viwanda na biashara? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi utaona jitihada kubwa ambazo zinafanywa na Serikali kwa kupitia mradi wa DMDP kuhakikisha kwamba Dar es Salam inajengeka, kwa maana ya miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ambayo ameisema Mheshimiwa Mbunge kuna jumla ya shilingi bilioni 260 kati ya shilingi bilioni 660 imetengwa kwa ajili ya mradi huu. Naomba nimwondoe hofu, katika mipango ambayo inafanywa na taratibu karibu zote zimekamilika; tukishakamilisha ujenzi wa barabara hiyo ambayo na mimi nimeenda kuitembelea tutaenda mpaka Kisarawe.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya barabara ambazo zina changamoto ya muda mrefu, lakini ni muhimu sana ni barabara ya Makongo kwa mantiki ya kwamba UCLAS, Makongo Juu kwenda Goba, hii barabara nimeuliza kwenye swali la TAMISEMI kwa sababu ni barabara ya halmashauri, lakini ina hudumiwa na TANROADS kwa mantiki ya ujenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba zoezi la tathimini ya kulipa fidia wananchi limeshakamilika, lakini lime stuck kwa muda mrefu. Sasa kwa sababu ya umuhimu wa hii barabara na ni barabara ya kimkakati kwa sababu inasadia kupunguza foleni wakati wa ujenzi wa madaraja pale njia ya Ubungo…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sasa Waziri aniambie; ni lini ujenzi wa barabara hii utakamilika kumalizia kipande ambacho kimeshaanzwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba katika ujenzi wa barabara kuna hatua mbalimbali na katika huu mradi wa DMDP lazima ipatikane no objection kwa kila hatua. Pale ambapo fidia inatolewa nafasi ili kama kuna malalamiko mengine ambayo yatakuwa yame-raise, baada ya kuwa sorted out ndipo tunaendelea na hatua ya pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Halima, na bahati nzuri swala hili tumekuwa tukiwasiliana hata na Mheshimiwa Susan Lymo naamini na yeye labla anaishi maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliongea na Meneja wa TARURA kwanza kufanya marekebisho kwa muda wakati wa ujenzi mwingine unasubiriwa. Naomba avute subira, ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa; lakini pia kusiwe na malalamiko kutoka kwa wananchi.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuiuliza Serikali; ni lini itajenga barabara itokayo Bunda kwenda Musoma Vijijini ili wananchi wa Kangetutya, Saragana, Bugoji na Kandelema wafaidike kwa sababu wakulima wanapolima mazao yao wanapata shida sana kusafiri kutoka Musoma Vijijini kwenda Bunda? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
M NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote kubwa zinajengwa; na nimepata fursa ya kwenda Mkoa wa Mara kuna kipande tumeanza kwa ajili ya kujenga daraja pale na yeye mwenyewe ni shuhuda kama atakuwa amepata nafasi ya kwenda hivi karibuni. Naomba nimhakikishie, Serikali ya Awamu ya Tano, suala la miundombinu ni kipaumbele chetu. Avute subira, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote zinajengwa.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Barabara za Jimbo la Ilala zote za Mjini ni mbaya, na tukamuita Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo akaja akashuhudia, wakaitwa watu wa TARURA wote wakashuhudia, lakini mpaka leo barabara za Kalenga, Mindu, Mchikichi, Pemba, Aggrey, Likoma, Bonde, Mali, Utete, Morogoro, Kikuyu, Mafuriko, pamoja na barabara ya Pemba; barabara hizi zote; na barabara zote hizi ndiyo sehemu ya uchumi wa Dar es Salaam na huchangia asilimia 70 ya mapato ya Taifa katika Taifa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ione umuhimu wa kuboresha kiundombinu hii ili wananchi waendelee kulipa kodi vizuri.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nawe ni shuhuda jinsi ambavyo Mheshimiwa Zungu anazifahamu barabara, amezitaja nyingi kweli kweli. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Zungu ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara ndani ya Jiji la Dar es Salaam zinajengwa na kuboreshwa kwa kiwango kikubwa. Ndiyo maana kwa kupitia mradi wa DMDP imetengwa jumla ya shilingi bilioni 660 na zitajengwa kilomita 210.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa barabara ambazo Mheshimiwa Zungu amezitaja zitakuwa ni miongoni mwa barabara ambazo zitajengwa. Tuko kwenye hatua nzuri, baada ya muda si mrefu tutakuwa tumeshaweka Mkandarasi kwa ajili ya kuanza kujenga barabara hizo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana pamoja na majibu haya ya Serikali Jimbo la Mbulu Vijijini lina Kata 18 na tuna kituo kimoja tu cha afya na kama alivyosema kwamba tumetenga maeneo na wananchi wameshakusanya material yaani mchanga, simenti na wengine tumeanza kujenga, je, Serikali itaongeza nini katika jitihada hizi za wananchi ambao wenyewe wameamua kujenga vituo vya afya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa kuwa wamekiri kwamba Zahanati ya Hayderer miundombinu yake haifai ili zahanati ile ikahuishwe ikawa kituo cha afya, je, uko tayari sasa kuja pale ili kuangalia namna gani na kutusaidia ili tukapata walau kituo cha pili katika Jimbo la Mbulu Vijijini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika majibu yangu ya msingi tunakubaliana kabisa na jithada zinazofanywa na wananchi katika kujiletea maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vituo vya afya kama kazi nzuri ambayo imeanzishwa na wananchi wa Jimbo la Mheshimiwa Flatei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee naomba nichukue fursa hii kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Flatei Massay jinsi ambavyo amekuwa akipigania wananchi wake kuhusiana na suala zima la afya, na sisi Serikali kwa kuunga mkono ndio maana katika hospitali 67 za Wilaya ambazo zinajengwa na wao ni wanufaika. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu na hasa kwa wananchi ambao tayari wameonesha jitihada zao katika kujenga vituo vya afya na zahanati sisi kama Serikali tutakuwa tayari kwenda kushirikiana na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini juu ya utayari wangu hata kabla yeye hajasema anajua kwamba mimi niko tayari kwenda kule kwake ili tuende tukaone kitu gani kiko site tuweze kushauri namna bora ya kuweza kupeleka huduma kwa wananchi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niweke rekodi sahihi; swali langu halijajibiwa, nimeuliza kilometa tano za lami zilizoahidiwa na Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni katika Kata ya Kyerwa. Hii ni kata ya mjini, ina wafanyabiashara wengi, ina shughuli nyingi za kibiashara lakini watu wanateseka na adha ya vumbi inayosababisha ajali mbalimbali za mabasi, boda boda na magari mengine.
Swali ni lini kilometa tano alizoahidi Mheshimiwa Rais katika Kata ya Nkwenda – kata ya kibiashara – zitajengwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tumeshuhudia taharuki na bomoa bomoa katika Kata hii ya Nkwenda ambayo hatuoni kama imetengewa bajeti lakini bomoa bomoa na X zinaendelea. Swali, wale wanaowekewa X na kubomolewa nyumba zao watapewa fidia kwa kuwa hakukuwa na ramani ya mpangomji na ramani sasa inawafuata watu wakiwepo pale; watapewa fidia katika maeneo yao ambayo yanakwenda kupitiwa na bomoa bomoa ya ujenzi wa barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika majibu yangu ya msingi, unapoanza kujenga kilometa tano ukaanza na kilometa moja tayari ulishaanza ujenzi kuelekea kilometa tano ambazo Mheshimiwa Rais ilikuwa ahadi yake. Kwa hiyo, nimemhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo wajibu wake ni kutekelezwa ndani ya miaka mitano na kuhakikisha kwamba ahadi hizo zinatekelezwa ndiyo maana tunaanza na kilometa moja. Ukijenga kilometa moja katika tano zinakuwa zimebaki kilometa nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia anauliza juu ya wananchi kulipwa fidia. Sheria iko wazi, kwa wale wananchi ambao wameifuata barabara ambayo; hatuwezi wakati huo huo tukataka maendeleo na wakati huo huo tukataka tubaki katika hali ile kabla ya maendeleo. Kwa hiyo, kwa wale ambao wameifuata barabara hawatalipwa na wale ambao barabara imewafuata watalipwa kwa mujibu wa sheria.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona na kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mheshimiwa Rais, mgombea wakati ule 2015 aliahidi Makambako Mjini kutupatia kilometa sita za lami; na kwa kuwa Serikali tayari imeanza kutupatia mita 150 ambazo tayari zimeshajengwa na mkandarasi ameondoka; na tayari tena atakuja kujenga mita 150. Kwa nini sasa mkandarasi huyu amekuwa akija mita 150 gharama itakuwa ni kubwa, kwa nini asianze kujenga kilometa sita zote kwa pamoja ili kukwepesha gharama ya Serikali isiwe kubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jah People (Mheshimiwa Deo Sanga), Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi, ahadi ambazo zilitolewa na Mheshimiwa Rais wakati akiomba kura kwa Watanzania ziko nyingi, na ziko za aina tofautitofauti. Zile ambazo zinahitaji fedha nyingi zinaratibiwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na zile nyingine ambazo ni idadi ndogo ya kilometa ambazo zinajengwa zinaratibiwa kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI na ndiyo kama hiyo ya Makambako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba kama ilikuwa ni kilometa sita na Mheshimiwa Mbunge anasema kwamba tayari tulishajenga mita 150 na nyingine 150, naomba nimhakikishie kwamba kabla ya miaka mitano kukamilika ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa kilometa sita tutakuwa tumekamilisha.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nakushukuru sana kwa kuniona; naomba niulize swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kaliua Mjini pale Mheshimiwa Rais aliahidi kilometa tano za lami ndani ya Mji wa Kaliua, na mwaka jana wakati amekuja kwenye ziara yake pia tulimkumbusha akasisitiza kwamba ahadi hiyo itekelezwe kwa wakati. Naomba kujua Serikali itaanza lini utekelezaji wa kilometa tano za lami ndani ya Mji wa Kaliua Center? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya msingi, ahadi zote za viongozi wakuu wa Kitaifa zitatekelezwa. Kwa kuanzia naomba niwaagize TARURA mkoani kwake na hasa Wilaya ya Kaliua wahakikishe kwamba wanatenga katika mwaka wa fedha 2018/2019 ili ahadi ya Mheshimiwa Rais ya Ujenzi wa kilometa tano ianze kutekelezwa mara moja.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hili swali la kuuliza kuhusu uwanja wa ndege na kuiomba Serikali ione umuhimu wa kuupandisha hadhi huu uwanja utoke kwenye Halmashauri na uende kwenye Tanzania Aviation Authority; kwa sababu kwa sasa hivi ilivyo kumkodisha Coastal Aviation kwa milioni 20 kwa mwaka anakuwa ana-monopolize na kodi ambazo anawataja aviation zingine wanavokuja kutoa pale ni nyingi sana; kwa hiyo Serikali tunapoteza mapato mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, ni kwa nini sasa Serikali haioni umuhimu wa kupandisha hadhi huu uwanja na kuukarabati kwa sababu tunapata watalii kutoka maeneo mbalimbali, lakini pia unaweza kutumika kwa ndege kutoka pale kwenda hata nchi jirani ya Kenya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwa nini sasa wameeleza hapa kwamba wamekarabati barabara ya kilometa 1.2, lakini kuna barabara ya kutoka Tarime kupita Magena unaenda mpaka Kata ya Mwema kule ambapo kuna daraja la Mto Moli ni bovu sana hata Clouds Tv walionesha…..
…linahatarisha maisha watu wanaotumia ile barabara. Ni lini sasa Serikali itaweza kujenga daraja lile la Mtomoli sambamba na ile barabara ambayo inaenda Magena kwenye huu uwanja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya kuomba kupandishwa uwanja huu kuchukuliwa na iwe miongoni mwa viwanja ambavyo vinamilikiwa kitaifa haina ubaya. Hata hivyo ni vizuri tukajua chimbuko la uwanja huu. Uwanja huu mwanzo ulikuwa unatumiwa na kampuni hii ambayo inajiita COGFA ambao wanajenga barabara ya kutoka Sirari kwenda Makutano. Na wao baada ya kumaliza matumizi yake walimkabidhi Mkuu wa Wilaya, lakini baadae bali katika kugawanyika Halmashauri ya Mji na halmashauri ya Tarime Town Council na DC ikaonekana kwamba uwanja ule ambao uko kilometa tisa ubaki chini ya umiliki. Ukitazama katika mkataba wao ambao ni suala la wao ndani ya Halmashauri, kwa sababu mkataba umeingiwa kati ya Coastal Aviation na Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo linaongeleka, kwa kadri watakavyopisha kwenye vikao vyao na wakaridhia kwamba sasa ownership ihame sisi kama Serikali hatuna ubishi na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya swali la pili la kujenga daraja, kama ambavo tumekuwa tukitengeneza miundombinu kwa kadri bajeti inavyoruhusu, naomba nimehakikishie Mbunge bajeti ikiruhusu tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba mazingira rafiki kwa ajili ya watalii kwenda mbuga yanajenga, ni pamoja na kujenga kwa daraja.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Soko la Kimataifa la Lemagwi ambalo lilikuwa limejengwa na baadaye kutelekezwa, liko Wilayani Tarime, ambalo lingeweza kusaidia kuuza mazao mbalimbali. Tungependa kujua, ni lini Serikali itamaliza kujenga hilo soko ambalo limetumia zaidi ya billions za Watanzania na baadae limetelekezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali wka kuzitaka halmashauri zote ambazo zina miradi ya kimkakati ambazo wana uhakika katika uwekezaji pesa inakwenda kupatikana ikiwa ni pamoja na Halmashauri ya kwao, ni vizuri wakahakikisha kwamba andiko linakamilika ili kama kuna sehemu ambayo Serikali inahitaji kuwekeza nguvu yake tujue exactly nini ambacho tunakwenda kukipata kama halmashauri kabla ya nguvu kubwa haijawekezwa huko.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali juu ya kituo hiki. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa kituo hiki kilijengwa siku nyingi tangu 1970; na kwa kuwa majengo mengi yamechakaa; na hivi karibuni, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano alipopita katika eneo hilo aliwaahidi Wanabunda wa kituo hiki kwamba kituo hiki kitakarabatiwa haraka; ni lini Serikali itakarabati kituo hiki ili kiweze kuwahudumia wananchi wa Bunda?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Makambako tuna kituo cha afya ambacho kinahudumia wananchi wa Mji wa Makambako; na kwa kuwa mwaka 2017 Serikali ilitupa fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba, hasa vya upasuaji na kwa sababu sasa hivi kituo hakina x-ray, ultrasound na vifaa tiba. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha ambazo iliahidi shilingi milioni 500, kwa ajili ya kununua vifaatiba na hela za kujengea wodi ili wananchi hawa wasipate adha ya kwenda kupimwa sehemu nyingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Ikizu ni miongoni mwa vituo bora kabisa katika Wilaya ya Bunda ambayo kinatoa huduma ya upasuaji. Pale wana mpaka ambulance na mortuary ya kisasa kabisa. Lakini pia naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ya kukarabati vituo vyetu vya afya vilivyochakaa bado iko pale pale. Kutegemeana na upatikanaji wa fedha, tutaendelea kufanya ukarabati na maboresho.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili Mheshimiwa Sanga anataka kujua lini vifaa kama x-ray pamoja na ultrasound vitapelekwa katika kituo chake cha afya cha Makambako? Naomba nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI imepeleka fedha MSD kwa ajili ya kununulia x-ray pamoja na ultrasound. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vyote vya afya vinavyokarabatiwa vinatoa huduma ya upasuaji pamoja na vipimo kwa kutumia x-ray. Kwa hiyo, nawataka wananchi wa Makambako wahakikishe katika ujenzi unaofanyika, pia na jengo la x-ray liwepo. (Makofi)
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii.
Kwanza kabisa naipongeza Serikali kwa kutupatia shilingi milioni 800 ambazo maboresho makubwa ya Hospitali ya Wilaya ya Nzega yanaendelea. Sasa nataka kuuliza kwamba Serikali mna mpango gani na Vituo vya Afya vya Itobo na Bukene ambavyo vina tatizo kubwa sana la wodi. Je, baada ya kumaliza maboresho ya Hospitali ya Wilaya, mtakuwa tayari sasa kuelekeza nguvu kwenye Vituo vya Afya vya Itobo na Bukene?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kimsingi tutakuwa tayari kama ambavyo tumekuwa tayari siku zote. Hatua kwa hatua tukimaliza vituo hivi ambavyo tumeanza navyo tutakwenda na Vituo vingine vya Afya.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mpanda Town Clinic ni kituo ambacho kinaisaidia sana Hospitali ya Manispaa ya Mpanda, lakini kwa bahati mbaya kituo hiki ilikuwa kikarabatiwe kwa kupitia fedha za ruzuku kwa maana ya miradi viporo. Naomba kuiuliza Serikali, ni lini watatusaidia fedha hiyo ili tuweze kukisaidia kituo hiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nilipata bahati ya kutembelea Mkoa wa Katavi na Manispaa ya Mpanda nimeitembelea. Pale jirani na stand, kuna ujenzi wa Kituo kipya cha Afya, lengo ni kuhakikisha kwamba msongamano katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda unapungua.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kapufi, naye ni shuhuda, tulikuwa wote pamoja; ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma ya afya inasogezwa kwa wananchi.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze tu kuweka taarifa sahihi kadri ya majibu ya Mheshimiwa Waziri hapa, kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Masasi ina Vituo vya Afya vinne tu ambapo viwili ni vya Serikali na viwili ni vya mission ya Wakatoliki vikiwemo Kituo cha Namombwe na Lukuledi na siyo vituo 33.
Mheshimiwa Spika, suala la gari la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Chiwale ambalo liliungua moto mwaka 2010, wananchi waliunguza moto pale na walioliunguza moto gari hilo siyo wananchi wote wa Chiwale isipokuwa ni watu wachache ambao hawakuwa na nia njema wakati huo, lakini Serikali inaonekana kwamba imekuwa ikitumia jambo hili kama adhabu kwa ajili ya watu wa Chiwale.
Mheshimiwa Spika, sasa nataka kupata kauli ya Serikali na tunafahamu kabisa kwamba mapato ya Halmashauri sasa hivi yamechukuliwa na Serikali Kuu, kwa hiyo, isingekuwa rahisi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Masasi kuanza kutenga pesa ukizingatia pia ahadi ya Waziri Mkuu wakati tunafanya uzinduzi wa wodi ya akina mama kwenye Hospitali ya Chiwale…
Mheshimiwa Spika, sasa swali langu, Serikali, pamoja na hili inalolieleza, vipi, inaweza kutekeleza ile ahadi ya Waziri Mkuu ya kuweza kuleta gari kwenye zahanati ya Chiwale?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama utakumbuka mwaka 2017 kwenye bajeti iliyopita, Serikali ilitenga shilingi milioni 70 kutoka kwenye basket fund kwa ajili ya kudhamini ujenzi wa Kituo cha Afya cha Lukuledi ambapo mpaka sasa hivi naongea hapa, wananchi wako pale wakijitolea pamoja na nguvu ya Ofisi ya Mfuko wa Mbunge. Sasa swali langu ni je, ni lini ahadi ya shilingi milioni 70 ya basket fund itapelekwa Lukuledi kwa ajili ya kuwasaidia na kuwaunga mkono wananchi wale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika majibu yangu ya msingi nimesema kuna vituo vya kutolea huduma za afya vitatu, sijasema vituo vya afya. Kwa hiyo, nilikuwa niko sahihi katika jibu nililokuwa nimetoa.
Mheshimiwa Spika, katika maswali yake mawili, kwanza anasema Halmashauri yake haina uwezo wa kutenga fedha kwa ajili ya kununua ambulance ambapo lengo la fedha hizo ni kwa ajili ya kusaidia wananchi wanaohitaji huduma ya afya.
Mheshimiwa Spika, ni jana tu nilikuwa naongea na Mkurugenzi wa Halmashauri; uwezo wa Halmashauri wanakusanya jumla ya shilingi bilioni 2.7. Nia ya dhati ikiwepo wakati inasubiriwa ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kutenga pesa kwa ajili ya kununua gari kwa ajili ya wagonjwa kutoka kwenye shilingi bilioni 2.7 inawezekana kabisa.
Mheshimiwa Spika, ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu itatekelezwa kwa kadri pesa zitakavyopatikana, lakini siyo vibaya kama wakatenga kutoka kwenye bilioni 2.7 kwa ajili ya ambulance.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anasema kwamba walishaanza ujenzi na tayari kuna ahadi ya shilingi milioni 70 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa zahanati au kituo cha afya.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge; ni azma ya Serikali inayoongozwa na CCM kuhakikisha kwamba huduma za afya zinaboreshwa na kusogezwa kwa wananchi. Kwa hiyo, avute subira. Azma yetu ndani ya miaka mitano ambayo ndiyo ahadi yetu na sisi kwa wananchi, tutatekeleza.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hapa swali alilouliza lilikuwa ni kuhusu kupandisha hadhi Kituo cha Afya na amesema wana mpango wa kujenga Hospitali ya Wilaya ambayo wanazidi kuiboresha, je, ni lini sasa kituo hiki ambacho Mheshimiwa amekitaja kitapewa uwezeshaji kama ambavyo tumeona katika vituo mbalimbali nchini ili na chenyewe sasa kiweze kujitosheleza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa katika Jimbo la Mlalo Halmashauri ya Lushoto, Zahanati ya Malindi na Zahanati ya Manolo zina miundombinu inayotosheleza kuwa na hadhi ya Vituo vya Afya na ukizingatia kwamba hizi ziko katika Tarafa ya Mtae ambayo haina hata kituo kimoja cha afya. Je, lini sasa Serikali itahakikisha inatusaidia katika ule mpango wa shilingi milioni mia nne mia tano ili Tarafa hii iweze kupata kituo cha afya chenye uhakika.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la msingi linauliza likiwa linataka suala zima la Hospitali ya Wilaya na katika majibu ambayo nimeyatoa nimeeleza jitihada ambazo zinafanywa na Serikali katika kujenga Hospitali ya Wilaya ndiyo maana kimetengwa kiasi cha shilingi bilioni 1.5 ili ujenzi wa hospitali hiyo ambayo eneo tayari limeshatengwa ekari 40 ianze kujengwa. Sasa katika swali lake la msingi anataka hicho kituo cha afya ambacho kina hadhi ya kituo cha afya, labda Mheshimiwa Mbunge anadhani kwamba hakijakamilika. Kituo cha Afya kimekamilika na ndiyo maana kimekuwa kikitumika kama Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la msingi la pili, kuhusiana na Jimboni kwake ambalo angependa zahanati ambazo ziko na zinafanya kazi zipandishwe hadhi zifanane na vituo vya afya au kuanza ujenzi wa vituo vya afya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni adhma ya Serikali kuhakikisha kwamba zahanati zinaendelea kuwepo lakini pia haiondoi haja ya kuwepo vituo vya afya. Wakati wowote ambapo pesa itapatikana hatutaacha kutizama maeneo ya kwake na ninaamini tutapata fursa pia kutembelea eneo la kwake.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Tabora Manispaa haina Hospitali ya Wilaya, je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu kukosekana kwa Hospitali ya Wilaya na hata kwenye bajeti hii haikuwekewa, je, nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, utakabaliana na mimi kwamba swali hili linaulizwa kwa mara ya tatu kama si mara ya nne, kuhusiana na suala zima la uwepo wa Hospitali ya Mkoa wa Tabora ili Hospitali ya Mkoa ya Kitete iweze kupata pahali pa kupumulia. Kama ambavyo imekuwa nikijibu ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba ili Hospitali ya Wilaya ambayo imeshaanza kujengwa, iendelee kujengwa. Ni suala tu la kibajeti, hali ikiruhusu hatuwezi kuacha kujenga Hospitali ya Wilaya ndani ya Manispaa ya Tabora ili Hospitali ya Kitete iweze kupumua.
MHE. ENG. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru kwa majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri yanayotia matumaini kwa wananchi wa Kata zote tano za Tarafa ya Itiso ambayo wanapata huduma pale pamoja na Wilaya ya jirani ya Chemba ambayo pia wanapata huduma katika Kituo cha Afya cha Haneti. Hata hivyo pamoja na majibu hayo mazuri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kituo hiki na chumba hiki kiweze kufanya kazi vizuri kunahitajika kuwe na vifaa tiba vinavyohudumia mle ndani. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba jengo linapoisha basi na vifaa tiba viweze kupatikana ili wananchi waweze kupata huduma?
Mheshimiwa Mwenyekitil, pili wataalam husika ni wachache sana. Hata katika Kituo cha Afya cha Haneti madaktari na wataalam wengine ni wachache. Je, Serikali ina mpango gani sasa kuhakikisha kwamba kituo na jengo hili litakapoikwisha la upasuaji wataalam pia wanakuwa wanapatikana wa kutosha wa kuweza kuwahudumia wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya swali la kwanza uwepo wa vifaa vya upasuaji na vifaa vingine pale ambapo Kituo cha Afya cha Haneti kitakuwa kimekamilika ili viweze kuanza kufanya kazi, naomba nimhakikishie, kwanza, katika Kituo cha Afya cha Haneti tayari vifaa vya upasuaji vimeshanunuliwa vipo tayari. Kwa hiyo tunasubiri tu kikishakamilika na vifaa vingine vitaongezwa ili kianze kufanya kazi kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anauliza kutaka kupata uhakika pale ambapo vituo vya afya vinakamilika wataalam/watumishi wawepo wa kutosha. Ni azma ya Serikali maana itakuwa hakuna sababu ya kumalizia majengo yakawa mazuri halafu tukakosa watu wakuweza kutoa huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba pale vituo vinavyokamilika na watumishi watapelekwa. Ndiyo maana hivi karibuni kuna nafasi ambazo zilishatangazwa kwa ajili ya watu wa afya waweze kuomba na waweze kuajiriwa.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Nishukuru majibu mazuri ya Serikali yenye dhamira ya kuona sasa wananchi wanapatiwa huduma ambazo zinakidhi. Kwa kuwa, Serikali imeona busara hii na kutoa ruzuku kwa Hospitali hii ya Mtakatifu Gaspar lakini gharama zake ni juu sana na sasa Serikali imeona ni vizuri ianze kujenga hospitali ya Wilaya katika Halmashauri ya Itigi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, katika kutekeleza Ilani ya CCM tunazo changamoto ambapo Serikali imetuletea pesa za kujenga kituo cha afya lakini gari la Kituo cha Afya ni dogo, wakati huo huo kuna Kituo cha Afya cha Mitundu ambacho ni kilometa zaidi ya 100 kutoka kituo cha afya kwenda Hospitali ya Wilaya ya Manyoni iliyopo sasa. Je, Serikali iko tayari kutoa gari la wagonjwa kusaidia kituo kile ili kupunguza gharama za wananchi wetu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Kituo cha Afya Rungwa ambacho kiko zaidi ya kilometa 200 kimeshakamilika. Je, Serikali iko tayari sasa kukifungua kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza anaongelea juu ya suala zima la upungufu wa magari kwa maana ya ambulance kwa ajili ya kituo cha afya alichokitaja ambacho anasema kipo karibia kilometa 100. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inapunguza adha kwa wananchi hasa wagonjwa, ndiyo maana gari zinapopatikana zimekuwa zikitolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pale magari yatakapokuwa yamepatikana tutaanza kupeleka maeneo yenye uhitaji mkubwa hasa yale ambayo yanahitaji kutembea umbali mrefu. Naamini na hicho alichosema Mheshimiwa Mbunge nasi pia tutazingatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anaulizia juu ya utayari wa Serikali kufungua kituo cha afya kilichokamilika. Essence ya kujenga kituo cha afya ni ili kiweze kutoa huduma kwa wananchi. Serikali kama mambo yote yamekamilika tuko tayari kuzindua kituo hicho cha afya. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri swali dogo la nyongeza. Ni lini Serikali itazuia wagombea Urais kutoa ahadi ambazo zinachukua muda mrefu kutekelezeka ikiwepo suala la zahanati na barabara? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, wagombea nafasi za Urais wanaenda kuuza sera kwa wananchi ili kwa sera hizo waweze kuchaguliwa. CCM ambao ndiyo tulichaguliwa na wananchi baada ya kuuza sera na ahadi zilizotolewa na Mheshimiwa Rais na katika kutekeleza ahadi za Mheshimiwa Rais mkataba wake na wananchi waliompa kura ni miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni shuhuda, tumekuwa tukipata fursa ya kujibu maswali juu ya maeneo mbalimbali ambayo ahadi za Mheshimiwa Rais zilishatekelezwa. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kuzuia ahadi hizo kwa sababu zimekuwa zikitekelezwa. (Makofi/Kicheko)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara kutoka Babati - Basodesh kuna korongo kubwa sana ambalo linawazuia watoto kwenda shule na kutokana na mvua hizi, ndiyo kabisa hali imekuwa mbaya. Je, Serikali ina mpango gani kuwasaidia watu hawa wa Hanang ili daraja au korongo hili likaweza kujengwa kwa sababu bajeti ya Halmashauri ya Hanang ni ndogo haiwezi kujenga barabara?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Hanang na Jimbo la Mbulu Vijijini lilikuwa pacha. Kuna barabara nyingine inayotoka Dongobesh kupitia Maretadu kwenda Haydom hapitiki kabisa kwa sababu ya mvua hizi ambazo zimekuwa nyingi maeneo ya kule Mbulu. Je, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ina mpango gani wa kusaidia kukarabati barabara hizi ambazo mvua nyingi zimeharibu kabisa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge mtakubaliana nami kwamba mvua zilizonyesha ni nyingi, mvua ni neema lakini wakati mwingine zikizidi pia zinaleta uharibifu mkubwa sana wa miundombinu. Kwa hiyo, kwa ujumla wake, naomba niwaagize Mameneja wa TARURA wa Wilaya zote mbili wakatazame uharibifu ulivyo, halafu waweze kushauri Serikali nini tuweze kufanya katika kusaidia ili wananchi waendelee kupata huduma.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi mvua za mwaka 2017 mwishoni na mwaka huu 2018 zimevuruga sana miundombinu katika Jimbo la Kondoa Mjini. Moja ya barabara iliyoharibika sana ni barabara ya Kingale ambapo mpaka daraja lenye mawasiliano makubwa sana kati ya Kingale na maeneo ya jirani lilivunjika. Daraja hilo limekuja kuangaliwa na watu wa TARURA Mkoa na watu wote wamelichunguza, mpaka sasa hivi bado halijafanyiwa kazi.
Je, ni lini sasa Serikali italeta mpango wa dharura wa kurudisha mawasiliano pale Kingale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba tumekuwa na mvua nyingi ambazo zimesababisha uharibifu mkubwa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anasema katika swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika pesa ya dharura ambayo ilikuwa imetengwa kwa ajili ya matengenezo ya dharura, theluthi mbili ya pesa hiyo imetumika katika kurudishia miundombinu katika Mkoa wa Dar es Salaam, kwa sababu uharibifu uliotokea kwa Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa mkubwa sana. Hata hivi leo hii navyoongea almost pesa yote iliyokuwa imetengwa ya dharura imeisha kwa sababu mvua zimenyesha, miundombinu mingi ikawa imeharibika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikubaliane na Mheshimiwa Sannda na sababu sasa hivi na mvua nazo hata huko Kondoa hazinyeshi, kabla hatujaanza utekelezaji wa hiyo bajeti ambayo tulipitishiwa na Waheshimiwa na Wabunge, kama Serikali tutaona kuna haja ya kuchukua hatua zozote endapo maeneo hayo hayapitiki, tutafanya hivyo ili wananchi waendelee kupata huduma.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi kama alivyosema Naibu Waziri kwamba mvua za mwaka huu na miaka mingine zimekuwa zikileta adha kubwa sana kwa Jiji la Dar es Salaam.
Nataka Serikali ituambie, wana utaratibu gani sasa kuhakikisha kwamba miundombinu hasa ile ya mwendokasi pale walipoweka Makao Makuu pale Jangwani, inahamishwa ili kuhakikisha kwamba wananchi wa Dar es Salaam wanapata usafiri bora, hasa ikizingatiwa kwamba Serikali iliwaondoa watu Jangwani lakini imejenga kituo kikubwa cha mwendokasi; ni lini mtakiondoa kituo kile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimetangulia kutoa majibu yangu, mvua za safari hii zimekuwa nyingi ukilinganisha na miaka ya nyuma. Katika swali lake anaongelea juu ya suala zima la kuondoa ile stand au tuite garage ya mabasi yaendayo kasi kwa maana ya pale Jangwani, lakini issue siyo kuiondoa bali kuhakikisha kwamba miundombinu ipi inakuwepo ili hata kama mvua zikinyesha pale pasiweze kuathirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna mpango mahsusi kwa ajili ya Jiji la Dar es Salaam wa kuhakikisha kwamba Bonde la Msimbazi linakuwa na miundombinu ambapo maji ambayo yatakuwa yanatoka kule juu yanaenda baharini kama ambavyo mkondo unaelekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa avute subira tarehe 20 Julai, kandarasi inafunguliwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miundombinu ile inakuwa na ukarabati ambao utakuwa ya uhakika kabisa. (Makofi)
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa walengwa wa mikopo hii ya asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri zetu wanapewa kwa makusudi ya kufanya biashara ili waweze kuzirejesha baada ya kupata faida. Je, walengwa hawa ambao ni wanawake, vijana na watu wenye ulemavu wametayarishwa kwa kiasi gani ili waweze kuelewa masharti ya mikopo hiyo, aina ya biashara wanazopaswa kufanya, lakini zaidi sana elimu ya ujasiriamali kwa sababu mwishowe watahitajika kurejesha kwa faida? Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kutokana na majibu ya Naibu Waziri kwamba malengo ya kutoa mikopo hii ni kuwapa watu wa hali ya chini sana katika nchi yetu; na kwa kuwa kuna baadhi ya kaya maskini hapa nchini ambazo zinaongozwa na wanaume pia ambao wanahitaji msaada, je, Serikali ina kauli gani kuhusu kaya hizo ambazo zinaongozwa na wanaume ambao wanahitaji pia kupata msaada kutokana na asilimia 10 ya mapato ya halmashauri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala zima la elimu, ni ukweli usiopingika, maana wanasema kwamba, ‘mali bila daftari hupotea bila taarifa,. Ni wajibu wa Maafisa Ushirika na Maafisa Ustawi wa Jamii kuhakikisha kwamba watu wetu wanapata elimu juu ya kuanzisha biashara na namna nzuri ya kuweza ku-keep record ili wajue hicho kiasi ambacho wanakopa kinatumikaje ili waweze kurejesha kwa wakati kitumike kwa wengine.
Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla yeye mwenyewe amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba elimu inatolewa. Si elimu tu peke yake lakini amekuwa akisimamia mfuko ambao umekuwa ukifanya vizuri katika eneo la Mkoa wa Manyara. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali la pili, ni imani yetu kwamba pale ambapo unamwezesha mama unaiwezesha familia. Ni matarajio yetu kwamba akina mama katika mikopo hii wanayopata hawawaachi waume zao pembeni, kwa hiyo tunakuwa tunaiwezesha familia kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba pale ambapo kuna ushirikiano kati ya baba na mama hakika familia hiyo husimama. Ni matarajio yetu kwamba baada ya kuwatosheleza akinama tutatizama pia upande wa akina baba kama haja itakuwepo.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mkoani Mwanza kuna eneo la wananchi limechukuliwa kwa ajili ya matumizi ya Ikulu ndogo ikiwemo na lile eneo lenye mradi wa UWT. Napenda kujua sasa ni lini Serikali itawafidia wananchi hao pamoja na taasisi ambazo maeneo yao yamechukuliwa ikizingatiwa wananchi hao wamesitisha shughuli za maendeleo kwa ajili ya kupisha zoezi hilo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili eneo la Bugosi, Kata ya Nyandoto, Wilayani Tarime, kuna eneo la wananchi limechukuliwa na Jeshi takribani miaka mitano ama zaidi. Napenda kujua sasa ni lini Serikali itawafidia wananchi hao ilhali tathmini ya eneo hilo tayari ilishafanyika? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mchafu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika eneo ambalo Mheshimiwa Mbunge analitaja ingekuwa vizuri tukapata fursa ya kwanza kujua chanzo cha tatizo kwa kujiridhisha ili pande zote tujue nini kinatakiwa kifanyike ili haki iweze kutendeka. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba hakuna kipande cha ardhi cha mwananchi kitachukuliwa bila kupata fidia. Kwa hiyo, katika hilo eneo ambalo amelitaja ni vizuri tukajiridhisha hasa tatizo ni nini ili wananchi kama wanastahili fidia waweze kupata.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anaelezea eneo ambalo liko Tarime anasema kwamba eneo hilo limechukuliwa na Jeshi. Itakuwa ni ngumu sana unless kama tumejiridhisha kwa sababu Jeshi maeneo ambayo imekuwa ikitwaa ardhi kuna utaratibu ambao unawekwa juu ya fidia na fidia imekuwa ikitolewa. Katika hili ambalo ni jipya ni vizuri Mheshimiwa Mbunge akatoa fursa Serikali tukajiridhisha hasa nini ambacho kimetokea mpaka Jeshi ikaonekana limetwaa eneo hilo bila fidia. Maana inawezekana wananchi ndiyo wamelifuata Jeshi au Jeshi limekuja baada ya eneo la wananchi. Kwa hiyo, ni vizuri kutizama pande zote mbili ili kuweza kutoa majibu ambayo ni sahihi.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, haya matatizo ya ardhi yanasaidiwa na Mabaraza yetu ya Kata na Wilaya kufanya kazi, lakini tuna tatizo kubwa kwa Wenyeviti wetu wa Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya kuhudumia Wilaya zaidi ya mbili au tatu na wakati mwingine Wenyeviti hao mikataba yao imekuwa ikiisha lakini haiwi renewed kwa wakati. Kwa mfano, Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya ya Babati ambaye anahudumia Mbulu, Hanang na maeneo mengine mkataba wake umeisha muda mrefu na wananchi wanapata shida. Naomba nifahamu, ni lini mkataba wa Mwenyekiti huyu na Wenyeviti wengine mta-renew ili wananchi wapate haki zao kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, itakuwa si vizuri sana tukaliongea suala hili in blanket maana kuna kesi na kesi si kwamba Tanzania nzima mikataba haijakuwa renewed. Ingekuwa vizuri baada ya kumaliza kipindi hiki tukajua exactly ni nini ambacho kimetokea kwa kesi yake ambayo ameisema na ingekuwa ni vizuri na mimi nikalijua ili tujue namna nzuri ya kuweza kulitatua ili wananchi hao waendelee kuhudumiwa kama ipasavyo.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, panapotokea migogoro hiyo basi wananchi wengi wanakimbilia kupata suluhu katika Mabaraza yetu ya Ardhi ya Kata, lakini uwezeshwaji ili kuwepo na ufanisi wa Mabaraza hayo umekuwa ukisuasua. Mabaraza haya yanategemea faini za wateja wake ili yaweze kujiendesha na halmashauri imekuwa haisaidii. Je, ni lini sasa Serikali itatia mkazo wa kuwezesha Mabaraza haya ili ufanisi uweze kupatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Paresso, nilitaka kusema Gekul maana wakati mwingine wanafanana, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kwamba uanzishwaji wa Mabaraza ya Ardhi ilikuwa ni kwa ajili ya kusaidia wananchi na hasa katika maeno ambayo wale wajumbe wanayafahamu vizuri kulikoni kwenda kwenye mambo ya kisheria. Tunachotarajia kwanza ni wao kwenda kubaini na kuweza kusuluhisha.
Mheshimiwa Spika, pia ni ukweli usiopingika kwamba baadhi ya Mabaraza wamekuwa wakitumia zile tozo ambazo wanatoza wananchi kama chanzo na wakati mwingine kumekuwa mpaka hata haki kutotendeka. Ni vizuri tukalitizama kwa ujumla wake, maeneo mengine wanafanya vizuri, katika maeneo ambayo hawafanyi vizuri na hasa kwa kuanzia wale wajumbe ambao wanachaguliwa kuwa katika lile Baraza, katika maeneo ambayo haki imetendeka wamekuwa wakifanya vizuri sana lakini maeneo mengine lazima tukubaliane kwamba kumekuwa na shida ni vizuri tukalitizama kwa ujumla wake ili tukafanya revision namna nzuri ya kuweza kuenenda na suala hili.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza, napenda kutumia fursa hii kuishukuru Serikali kwa kutupatia fedha hizo shilingi milioni 500 na ni kweli Mkandarasi G.S Contractor yupo site.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nazungumza kwamba tuna baadhi ya vijiji wananchi wa Tanzania walioko kule hawajawahi kuona gari, baiskeli wala pikipiki, hiyo imeshuhudiwa hata na Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Nditiye tulipokuwa naye kule. Je, baada ya kuwa tayari kipande hiki kidogo tumeshakipata, TARURA ina mpango gani sasa wa kuhakikisha inafanya kazi hiyo kwa haraka ili Vijiji vya Makonde, Kilondo, Nsele, Lumbila, Nkanda, Nsisi na Lifuma viweze kupata barabara? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika swali la msingi, kazi ambayo inaenda kufanyika ni kufanya usanifu kujua gharama ambazo zitatumika katika ujenzi wa barabara hii ni kiasi gani ili hatua ya pili iweze kufuata. Pia mimi mwenyewe nimepata fursa ya kutembelea Wilaya ya Ludewa, Jimboni kwa Mheshimiwa, kama kuna maeneo ambayo jiografia ni changamoto ni pamoja na eneo la Ludewa, ndiyo maana unaona kwamba kipande kidogo kinagharimu kiasi kikubwa cha fedha kama hivyo ambavyo nimetaja katika jibu langu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, maeneo ya Lupingo ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba yanafikika kwa njia ya barabara. Avute subira, nia ya Serikali ni njema yeye mwenyewe anashuhudia, naomba tuvumiliane hili litakamilika kwa wakati. (Makofi)
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; wananchi wa Mtunda – Kikale -Myuyu bado wanapata shida kwani njia ile haipitiki kabisa kutokana na mvua nyingi zilizonyesha. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya ukarabati huo kwa haraka ili barabara hiyo iweze kutoa huduma?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, barabara ya kutoka Bungu - Msolo nayo haipitiki kabisa, tena hatari zaidi kuna shimo kubwa pale Bungu ambalo linaweza likakata mawasiliano baina ya wananchi wa Bungu na Msolo. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati barabara hiyo ili wananchi hawa sasa wapeleke mazao yao sokoni na wapate faida haraka iwezekanavyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kutembelea Jimboni kwa Mheshimiwa Mbunge, nikafika mpaka Delta na changamoto anazozitaja nazifahamu. Naomba nitumie fursa hii kumwagiza Meneja wa TARURA aende site akatazame kilichopo ili aweze kutushauri nini kifanyike ili wananchi wa Jimbo analolisema Mheshimiwa Mbunge wasije wakapata adha ya kukosa usafiri ili mazao yao yaweze kufika sokoni. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali ndogo la nyongeza. Ahadi hizi ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne ziko nyingi nchi nzima na kwa kweli zipo ambazo hazijatekelezwa kabisa, ikiwemo ujenzi wa kilomita mbili za lami katika Mji wa Karatu. Ahadi hiyo ilitiliwa msisitizo na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano akasema ataongeza kilomita nane jumla ziwe kilomita 10, lakini mpaka leo utekelezaji haujafanyika. Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kwamba kuna ahadi ambazo zimetolewa na Marais waliotangulia na katika utaratibu wa kawaida ni kupokezana kijiti, pale ambapo mwenzako ametekeleza yale ambayo hakuyamaliza wewe unahakikisha unayachukua na wewe unaongeza ahadi za kwako ili kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Paresso ni azma ya Serikali ndani ya kipindi cha miaka mitano ambayo ndiyo mkataba wa Mheshimiwa Rais na wapiga kura wake, barabara yake hiyo itaweza kutekelezwa kama ambavyo ahadi ya Mheshimiwa Rais ilivyoahidiwa.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kata ya Kapalamsenga sasa hivi iko kisiwani kwa kukosa miundombinu baada ya mvua zilizonyesha kuharibu kabisa miundombinu ya barabara. Serikali ina mpango gani wa kuharakisha kuifanyia matengenezo barabara hiyo ambayo kimsingi inawasaidia kwa ajili ya shughuli za maendeleo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba mvua za safari hii zimekuwa nyingi pamoja na neema ambayo inasababishwa na mvua lakini ni ukweli usiopingika kwamba barabara zetu nyingi zimeharibika. Naomba nitumie fursa hii nimuagize Meneja wa TARURA aende huko barabara ya Kapalamsenga ili akatizame uhalisia na nini ambacho tunaweza tukafanya ili wananchi waendelee kupata huduma. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kwa kumshukuru sana Makamu wa Rais alipokuwa amekuja kwenye jimbo langu na mimi nilimwomba Ambulance siku ile na utekelezaji umefanyika nashukuru sana. Swali langu la kwanza kule jimboni kwangu nina vituo vya afya kama vitatu ambavyo viko vijijini sana hakuna magari kwa mfano pale Mninga na Mtwango ni vituo vikubwa sasa. Je, Serikali itanisaidia tena kuniletea (Ambulance katika hivyo vijiji viwili ambao wananchi wanapata shida sana?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nina tatizo kubwa sana la watumishi wa Afya kwenye vituo vyangu vya afya na zahanati kwenye jimbo langu. Je, Wizara ya Afya ina utaratibu gani wa kuhakikisha kwamba watumishi wa Afya tunaweza kuwapata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza kwa niaba ya Serikali naomba nipokee shukrani ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Mbunge. Katika suala lake la kwanza, anaongelea vituo vya afya vingine viwili ambavyo viko mbali sana na vina uhitaji mkubwa wa magari ya Ambulance.
Mheshimiwa Spika, naomba nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali pale ambapo gari zinapatikana tutazisambaza na hasa tutazingatia maeneo yenye uhitaji mkubwa sana. Sasa kama na eneo la kwake litakuwa miongoni mwa hayo maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa hakika sisi tutatekeleza hilo, lakini ni vizuri pia akatambua kwamba kuna baadhi ya maeneo ambayo hawakupata hata hiyo gari ambayo yeye amepata kwa hiyo kwa kadri gari zitakapopatika tutafuata uwiano unaotakiwa ili haki iweze kutendeka.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anaongelea juu ya vituo vyake vya afya kutokuwa na watumishi wa kutosha, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge sasa hivi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeshatangaza nafasi 6,180,000 na naamini pale ambapo watakuwa wameajiriwa na eneo la kwake litaweza kufikiriwa kupelekewa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kufuatia majibu ya Serikali tayari barabara hii imetumia zaidi ya milioni 439.8 katika jitihada ya kutaka kuifungua. hata hivyo, mwaka huu haijatengewa fedha na wanasema itaendelea kuitengea fedha kadri fedha itakavyozidi kupatikana. Je, Serikali haioni kwamba kwa kufanya hivi inachelewa na fedha ambazo tayari imesha-invest kwenye barabara hizi zitakosa thamani?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kufuatia mvua nyingi zilizonyesha katika Mkoa wa Rukwa kuna barabara katika Jimbo la Nkasi Kusini zimefunga kabisa. Barabara hizo ni pamoja na Kisula - Malongo Junction - Katongolo- Namasi- Ninde - Kanakala na tayari TARURA imeleta taarifa ya orodha ya barabara hii. Je, ni lini fedha sasa zitatolewa kwa ajili ya kwenda kurudisha miundombinu ili iweze kutumika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, naomba kwanza uniruhusu kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Mipata barabara hii amekuwa akiipigania kwa nguvu zake zote na ndiyo maana Serikali imesikia kilio chake na hicho kiasi cha pesa kikaanza kutumika.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie kama ambavyo yeye mwenyewe amesema itakuwa si busara kwa Serikali kuweza pesa bila kupata matunda kwa sababu matunda yanayotarajiwa ni barabara kufunguka. Hata hivyo, naye atakubaliana nami kwamba barabara hii haikuwepo kabisa na kazi kubwa ambayo imekwishafanya kuhusiana na ujenzi wa madaraja pamoja na yale makalvati hakika pesa ikipatikana kipande ambacho kimebaki kitaweza kufunguliwa na wananchi waweze kupita kwenye hiyo barabara.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anaongelea baada ya mvua kunyesha kumekuwa na uharibifu katika barabara hizo ambazo amezitaja na bahati nzuri TARURA walishaleta makisio ya nini ambacho kinatakiwa kutumika. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pesa ambazo zilitengwa kwa ajili ya emergence almost zote zilishakwisha na theluthi mbili ya pesa hizo zilitumika katika kurudishia miundombinu katika Mkoa wa Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, pia naomba nimhakikishie kwa sababu bajeti ilishapitishwa naamini muda siyo mrefu pesa ikianza kupatikana na eneo la kwake litaweza kufunguliwa hizo barabara.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa kweli leo nimefurahi kidogo. Naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri amenijibu vizuri. Naomba nimuulize maswali mawili madogo ya nyongeza:
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, sera hii inalenga kutatua changamoto inayowapata wananchi kuhusu mitazamo mbalimbali lakini umesema pia sera hii inalenga kuwakopesha wanavikundi na mtu mmoja mmoja, swali langu ni kwamba; ni kwa nini sasa Halmashauri nyingi zimekuwa zikiwalazimisha wananchi wakope wakiwa kwenye vikundi vya watu watano na kuendelea, jambo ambalo kimsingi linamnyima mkopaji mmoja mmoja mwenye uwezo wa kukopa ambaye anaweza akajidhamini ili aweze kujiendeleza katika maisha yake?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, naishukuru Serikali yangu kwa sababu imeweza kuondoa riba katika hii mikopo ambayo imekuwa ikitolewa na Halmashauri asilimia kumi, lakini, ni kwa nini sasa, bado tunasema kwamba, kwa mfano kwenye Mifuko ya Akinamama na Vijana, wazee na wanaume hawapati mikopo hii, jambo ambalo tunaweza tukawakopesha na wakaweza kuendeleza mifuko hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza kipengele cha kwanza alichouliza Mheshimiwa Pudenciana Kikwembe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika swali lake anapendekeza ingefaa tukaanza kum-address mtu mmoja mmoja badala ya vikundi ambalo kimsingi na yeye mwenyewe atakubaliana na mimi na hata ukienda kule kwake, vikundi kwa maana ya ushirika ndiyo hasa njia ya kuweza kututoa sisi wanyonge. Naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge kuwa vyovyote, yule ambaye ana uwezo wa kuweza ku-access mabenki, window hiyo ipo, lakini katika hii pesa ambayo inatolewa na Serikali ni vizuri kwanza tukajikita katika vikundi maana tukisaidia vikundi tunasaidia watu walio wengi zaidi.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Spika, katika utaratibu wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, Serikali inachokifanya ni kuona namna ya kuweza kuyagusa makundi yote kwa wakati mmoja. Ndiyo maana pamoja na kwamba tunayo Mifuko ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi lakini pia tunayo mifuko maalum kwa ajili ya akinamama na vijana, lakini kundi la wazee na watu wengine ambao hawadondokei katika sifa hizo, wenyewe pia kupitia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi wanayo fursa ya kwenda kukopeshwa mtu mmoja mmoja au kupitia vikundi pia.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba bado hata kama kuna mzee na mtu mwingine yeyote ambaye anahitaji kupata mikopo hii, hata kama hadondokei katika kundi la vijana na akinamama lakini fursa hiyo ipo kupitia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambayo ipo 19 na imekuwa ikifanya kazi hiyo kuwawezesha wananchi kiuchumi.
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kumekuwa kuna hamasa ya uhamasishaji mkubwa sana kwa wananchi wetu kujiunga na vikundi hivi ili waweze kupata mikopo hii asilimia 10 kutoka kwenye Halmashauri zetu, lakini kiuhalisia Halmashauri nyingi mikopo hii haitoki. Nataka kujua, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha Halmashauri zetu ili mikopo hii iweze kutoka na akinamama, wazee na watoto waweze kupata mikopo hii kama inavyoonekana? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, swali hili limekuwa likijirudia mara kwa mara na majibu ambayo tumekuwa tukitoa, tumekuwa tukielekeza kwamba wakati tunakuja kuhitimisha bajeti kuna kipengele ambacho kitaingizwa katika Finance Bill ambacho kitamlazimisha kila Mkurugenzi kuhakikisha kwamba pesa hizi zinatengwa na zisipotengwa sheria zitachukuliwa ili kutoa adhabu kwa wale wote ambao hawatatimiza takwa hili la kisheria. Kwa sasa hivi, imekuwa ni kama option lakini tutakuja na kipengele ambacho kitamlazimisha kila Mkurugenzi a-make sure kwamba pesa hizi zinatengwa.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Spika, nakushuru. Swali la kwanza, kwa kuwa barabara hii ya Buhekela-Miswaki-Loya mpaka Iyumbu na ile barabara ya Igunga-Itumba-Simbo ni barabara ambazo zinapita kwenye Mbuga ya Wembele mahali ambapo ni lazima ujenge tuta kubwa ili barabara iwezekane siyo kuchonga, kwa hiyo, kuna madaraja mengi yanahitajika kujengwa.
Mheshimiwa Spika, Sh.225,000,000 za barabara ya Iyumbu na zile Sh.297,000,000 za barabara ya Itumba hazitoshi kabisa kuzijenga barabara hizi. Waziri anatoa commitment gani kuhusu kuongeza bajeti ili kujenga hii barabara kwa kiwango ambacho zitaweza kupitika wakati wowote?
Swali la pili, kwa kuwa ile barabara ya Igunga-Itumba- Loya kipande cha Itumba - Loya hakina fedha, kwa sababu inaenda Simbo kwanza. Ni lini basi Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kile kipande cha Itumba-Loya? Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli swali hili amekuwa akiuliza sana kuhusu kipande hicho cha Mbuga ya Wembele ambayo inahitaji special consideration na ni ukweli usiopingika kwamba inahitaji bajeti kubwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama Serikali tunalitambua hili, lakini kinachogomba ni suala la bajeti, pale hali itakavyokuwa imeimarika hatutasahau kwa sababu eneo lile linahitaji pesa nyingi. Naamini katika bajeti zijazo, kabla hatujafika 2020 tutakuwa tumeshaikamilisha. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mara nyingi Mawaziri wetu hapa Bungeni wamekuwa wakituambia kwamba ahadi ya Rais ni sheria na lazima itekelezwe. Sasa kupandisha hadhi Kituo cha Afya cha Palestina kuwa Hospitali ni ahadi na agizo la Mheshimiwa Rais. Sasa ni kwa sababu gani badala ya Serikali kutekeleza ahadi hii, inafanya maboresho?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Kituo cha Afya cha Tarakea katika Wilaya ya Rombo kinachukua wagonjwa wengi sana kutokana na eneo kubwa na wagonjwa wengine kutoka nchi jirani ya Kenya, lakini hakina incinerator, hakina mortuary, vilevile kilikuwa hakina uzio lakini Mbunge akajitahidi kwa fedha za Mfuko wa Jimbo kujenga uzio.
Sasa je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufika Rombo kutembelea kituo kile ili tushauriane naye namna ya kukiboresha kiweze kuhimili idadi kubwa ya wagonjwa ambao wanakwenda kwenye kile kituo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi, Serikali tunakiri juu ya umuhimu wa Kituo cha Afya cha Sinza pale Palestina, lakini ni ukweli usiopingika kwamba ili Kituo cha Afya kiwe Hospitali ya Wilaya kuna suala zima la eneo ambalo katika jibu langu la msingi nimemwambia kwamba tunahitaji ekari 25. Sasa ukienda katika kile Kituo cha Afya cha Palestina, eneo hilo halipo na ndiyo maana katika maboresho ambayo yanaendelea ni pamoja na kutenga shilingi milioni 160 ili kuweza kuwa na hadhi ya kufanana na Kituo cha Afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba tunapata changamoto katika Vituo vya Afya vilivyo Mijini, kitu ambacho kinakosekana ni jina lipi tutumie? Kwa sababu vinakuwa na hadhi zaidi ya Vituo vya Afya, lakini vinakuwa havijafikia kuwa Hospitali za Wilaya. Ndiyo maana nimesema kwamba ni vizuri Manispaa wakatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, kama Serikali tuko tayari na wala hatupingani na kile ambacho Mheshimiwa Rais alielekeza kwa wakati ule, lakini changamoto ya ardhi ndiyo inayotusababisha tuseme kwamba ni vizuri likatengwa eneo lingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, Mheshimiwa Selasini anataka utayari wangu kwenda kutazama Kituo cha Afya Tarakea. Naomba nimhakikishie, kama ambavyo nimefanya ziara kwenda Kituo cha Afya cha Kiaseri kule, niko tayari kufika hata Tarakea kwa kadri muda unavyokuwa umeruhusu.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyopo Ubungo inafanana kabisa na changamoto iliyopo Jimbo la Mbulu Vijijini. Tuna kituo kimoja tu cha afya Jimbo zima; je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutuongezea angalau kituo kimoja ili katika huduma za afya jimboni, pakawa na hali ya kuwasaidia wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyopo kwenye Kituo cha Afya katika swali la msingi, ni suala la eneo, lakini kwake yeye eneo siyo tatizo kama ambavyo iko Sinza, Palestina pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kwa dhati kabisa ya moyo wangu nimpongeze Mheshimiwa Flatei Massay kwa jinsi ambavyo amekuwa akilipigania Jimbo lake, amehakikisha kwamba Halmashauri inajengwa lakini pia ni miongoni mwa maeneo ambayo yanakwenda kujengewa Hospitali za Wilaya. Naomba nimhakikishie kwa dhati hiyo hiyo ambayo Serikali imeonesha kuhakikisha kwamba tunajenga Hospitali za Wilaya, ni azma yetu pia kuhakikisha kwamba tunajenga Vituo vya Afya vya kutosha na kwa kadri bajeti itakavyokuwa imeruhusu hakika hatutasahau eneo la kwake. (Makofi)
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Katika mwaka wa fedha unaokuja, Serikali imetenga fedha za kujenga Hospitali za Wilaya kwenye maeneo 67, lakini pia ni wazi zipo Wilaya nyingi ambazo bado hazina Hospitali ya Wilaya ikiwemo Wilaya yangu ya Karatu. Ni lini sasa wananchi wa Karatu wategemee kujengewa Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekuwa nikijibu hapa, kuanza na Hospitali za Wilaya 67 tafsiri yake ni kwamba zikikamilika hizo tutakwenda kujenga nyingine. Ni azma ya Serikali inayoongozwa na CCM kuhakikisha kwamba Wilaya zote ambazo hazina Hospitali za Wilaya baada ya kumaliza hizi 67 tutakwenda hatua nyingine ya kwenda kuzijengea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, bajeti ndiyo imepita, tumwombe Mwenyezi Mungu makusanyo yetu yaende vizuri, tukimaliza 67 tutakwenda hatua ya pili.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, mwaka 2014 alipotembelea Jimbo la Tunduru Kusini alitembelea katika Kijiji cha Mbesa ambapo kuna Hospitali ya Mission pale. Hospitali ile inatoa huduma kubwa kuliko Hospitali ya Wilaya na Mheshimiwa Rais aliahidi kuipandisha daraja hospitali ile kuwa Hospitali Teule. Je, ni lini hospitali ile itapewa hadhi ya kuwa Hospitali Teule ili iweze kuendelea kutoa huduma vizuri?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni Hospitali ya Mission ya Mbesa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekuwa nikijibu na ambavyo nimejibu leo, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo ambayo hakuna Hospitali za Wilaya zinakwenda kujengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni azma ya Serikali kwa kushirikiana na Taasisi za Dini na Mashirika mengine pale ambapo sasa hivi hatuna Hospitali Teule, tunatumia zile ambazo zipo ili zifanye kazi kwa muda tu kama Hospitali Teule. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunakuwa na hospitali zetu za Serikali na zile za Mashirika ya Dini pale ambapo tutakuwa tumejenga za Serikali wabaki wakiendesha kwao na sisi Serikali tuwe na za kwetu tukifanya kazi kama Serikali. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu kumshauri Mheshimiwa Mpakate, ili hospitali binafsi au ya Shirika la Dini ifanywe kuwa DDH sasa hivi tumeshusha madaraka haya kwenye Halmashauri husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Halmashauri ndiyo itafanya majadiliano na makubaliano na hospitali ile na tumeelekeza kuwe na mkataba wa muda maalum, kwamba Halmashauri ya Tunduru inaamua kuingia makubaliano na hospitali hii ili iwe Hospitali Teule ya Halmashauri na mkishakubaliana ndiyo mnaleta taarifa hizi TAMISEMI na Wizara ya Afya. Kwa hiyo, tutazitambua rasmi sasa kuwa ni Hospitali Teule ya Halmashauri husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, niseme tunatoka kwenye Hospitali za Wilaya, tunakwenda kwenye Hospitali ya Halmashauri. Kwa hiyo, sasa hivi kila Halmashauri itakuwa na Hospitali badala ya kuwa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama kuna Wilaya zina Halmashauri mbili, zote zinapaswa kuwa na Hospitali ya Halmashauri ambayo ni ngazi ya kwanza ya Hospitali. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kinachoendelea kwa sasa katika Kituo cha Afya cha Mlandizi ni kuelemewa na lundo la wagonjwa, hususan upande wa afya ya uzazi. Ndani ya mwezi mmoja kuna wanawake zaidi ya 250 wanaojifungua. Idadi hii ni mara tatu ya walengwa wa Kituo hiko cha Afya cha Mlandizi, kitu ambacho kinapelekea kituo chetu kuwa na mahitaji makubwa ya matumizi ya dawa, vifaa tiba na huduma za kujifungua. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, sasa napenda kujua, wakati huu ambao hatuna Hospitali ya Wilaya na Serikali haina mpango wa kujenga Hospitali hiyo ya Wilaya: Je, Serikali itakuwa tayari kutupatia fungu maalum la fedha kila mwaka kwa ajili ya huduma hii ya afya ya uzazi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kufuatia ongezeko hilo la wagonjwa kuwa mara tatu ya walengwa wa Kituo hicho cha Afya na kupelekea kituo chetu kuwa na deni kubwa takriban shilingi milioni 83 linalojumuisha matumizi ya dawa, vifaatiba, huduma ya uzazi na huduma nyingine, nangependa kujua, sasa Serikali itatusaidiaje ku-clear deni hilo, ukizingatia idadi hiyo ya fedha au kiasi hicho cha fedha ni mara mbili, tatu, nne mpaka tano ya mapato yote ya Kituo cha Afya cha Mlandizi? (Makofi) Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa nakushukuru. Katika jibu langu la msingi, nimesema kwamba Serikali imeona uhitaji wa kujenga Hospitali ya Wilaya na tayari katika bajeti ya 2018/2019 tumetenga shilingi bilioni 1.5, ni kwa sababu tunatambua umuhimu na uhitaji mkubwa sana wa wananchi kwa suala zima la Afya. Kwa hiyo, tuko tayari na ndiyo maana tunajua kabisa kuna kuelemewa ndiyo maana tunaenda kujenga Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anauliza, tunafanyaje katika kuwasaidia deni la jumla kama shilingi milioni 80? Ni vizuri kwanza tukajua chimbuko la deni hili nini na tukikaa baada ya kipindi cha maswali na majibu, tujue tatizo ni nini ili tuweze kusaidiana ili wananchi waendelee kupata huduma, lakini wakiwa wamevuta subira, Serikali yao ya CCM inawajali na ndiyo maana tunaenda kujenga Hospitali ya Wilaya.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami nataka niombe tu kwamba Kituo cha Afya cha Kata ya Vunta, Tarafa ya Mamba Vunta kimepandishwa hadhi kuwa Kituo cha Afya takriban miaka 10 iliyopita, lakini hakijafunguliwa rasmi kutokana na kwamba kilikuwa hakijapata ukarabati unaofaa.
Mheshimiwa Spika, pamoja kwamba tunashukuru Serikali ilipeleka Ambulance, namwomba Mheshimiwa Waziri kwamba ni lini Kituo hiki kitafunguliwa rasmi ili kitambulikane kwamba kweli ni Kituo cha Afya cha Tarafa ya Mamba Vunta yenye kata tano? Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwa sababu kuna sifa ya zahanati kupanda kutoka zahanati kuwa kituo cha afya, naye mwenyewe amekiri, ingekuwa vizuri baada ya kutembelea eneo hilo ambalo mimi nipo tayari, ili tukaone kama kweli inakidhi haja ya kuwa Kituo cha Afya itakuwa ni furaha kwangu mie kuhakikisha kwamba inapata hadhi ya kuwa Kituo cha Afya kwa mujibu wa kukidhi vigezo ambavyo vimewekwa ili kiweze kuwa Kituo cha Afya.

Kimeshapandishwa? Kama tayari kimeshapandishwa, maana yake kuna baadhi ya taratibu ambazo hazijafuatwa. Naomba tukishamaliza hiki kipindi cha maswali na majibu, nipate fursa ili tuweze kuongea na DMO tujue hasa nini ambacho kimetokea kama tayari kimeshapandishwa, lakini hakiwi treated kama Kituo cha Afya.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Hapa naweza nikasema ni pale ambapo Golikipa wa Simba anapigiwa shuti la penati na mshambuliaji wa Yanga halafu yeye anaenda kushoto goli linaingia kulia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, majibu yaliyotolewa na Serikali pamoja na shukrani zote, lakini kidogo yamekwenda tofauti na malengo ya swali lenyewe. Huu utaratibu wa Hospitali Tembezi tumekuwa tukiufanya hasa sisi wenyewe Wabunge tukishirikiana na Ofisi ya Mkoa. Tumefanya mara kadhaa, kama mara tatu na tunatarajia tena mwezi wa Septemba, 2018 tutapata nyingine kutoka Marekani.
Mheshimiwa Spika, nilichokuwa nikitarajia hapa ni ubunifu huu tulioanza nao kutokana na uchache wa huduma za kibingwa lakini pia na huduma nyingine za afya, kwenye ngazi ya Halmashauri na kwenye ngazi ya Wilaya tuupeleke kwenye vijiji, ndiyo maana niliainisha vijiji vingi ambavyo tunavizungumzia hapa.
Mheshimiwa Spika, kwa kawaida tumekuwa tunachukua gari la chanjo na mengineyo ya miradi kufikisha huduma za kliniki za watoto, chanjo, huduma za akinamama wale, lakini sasa zinafanyika nje kwenye uwazi, jambo ambalo halina staha sana, ndiyo maana tukawa tunahitaji Kliniki Tembezi. Huu ni ubunifu tuliofanya kwenye ngazi ya Wilaya, sasa tuufanye kwenye ngazi ya Vijiji. Je Serikali haioni umuhimu wa kuenzi na kuiga ubunifu huu kwenye ngazi ya vijiji? Hilo ni swali la kwanza.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuweza kujenga Zahanati kwenye kila Kijiji kama ilivyo sera yetu, gharama yake ni kubwa sana na haya maeneo yote niliyoainishwa unaweza ukazungumzia maeneo matano mpaka sita ambapo ukipata gari moja la namna hiyo la Kliniki Tembezi, linaweza likakusaidia kuweza kumaliza huduma ya kujenga Zahanati nne. Je, ni lini basi, na kwa kuwa tunafahamu uwezo wetu ni mdogo bora tufanye...
Eeh! Mheshimiwa Spika, ni lini basi, Serikali itaiga ubunifu huu na kutuletea Mobile Clinic Van kwa ajili ya maeneo yetu ya Kondoa? (Makofi
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu kwanza nimpongeze Mheshimiwa Sannda kwa jinsi ambavyo amekuwa akipigania wananchi wake kuhusiana na suala zima la afya. Wiki iliyopita alikuwa anaongelea juu ya suala la gari la wagonjwa, lakini leo anaongelea juu ya Mobile Clinic.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake alilenga gari linalotembea kwa ajili ya kutoa huduma. Sasa kwa namna ambavyo swali limekuja ndiyo maana anasema ni kama tumehamisha goli, lakini siyo nia ya Serikali kuhamisha magoli kwa sababu majibu yote tunayo.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anauliza uwezekano wa kuiga hili jambo zuri ili kuvipunguzia vijiji vingi badala ya kufuata huduma maeneo ya mbali. Naomba tukubalianae na Mheshimiwa Sannda kwamba ni nia ya Serikali, pale ambapo uwezo unakuwa umeruhusu hatuna sababu ya kutowapelekea wananchi huduma jirani yao.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anaomba tuige utaratibu mzuri ili kuwa na Mobile Clinic Van. Utakubaliana nasi kwamba wananchi wengi wamejitokeza, wametoa nguvu zao katika ujenzi wa Zahanati na Vituo vya Afya. Pamoja na wazo jema hili, lakini itakuwa siyo busara nguvu ile ambayo imetumiwa na wananchi tukai-dump halafu tukaanzisha jambo lingine. Kwa kadri nafasi itakaporuhusu na nguvu ya kibajeti ikiruhusu, wazo hili ni jema, naomba tulichukue kama Serikali kulifanyia kazi kwa siku za usoni. (Makofi)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali imekiri kuwa ilitenga shilingi bilioni mbili kwa mwaka 2017/2018, lakini ikapeleka kiasi cha fedha shilingi bilioni moja. Mkoa umejiwekea malengo ya kumaliza jengo hili ifikapo mwaka 2020 lakini Serikali inapeleka fedha kidogo kidogo. Pia kwa mwaka 2018/2019 Serikali tumeona tena imetenga kiasi cha fedha shilingi bilioni mbili, uzoefu umekuwa ukionesha kwamba fedha zinapelekwa kidogo kidogo na hivyo kukwamisha ukamilishaji wa majengo mengi ambayo yanakuwa yanajengwa katika hospitali zetu za mikoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, je, Serikali ina mpango gani mkakati wa kuhakikisha kuwa fedha hizi ambazo zimetengwa kwa mwaka 2018/2019 zinapelekwa zote lakini pia fedha ambazo zilitengwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018, bilioni moja iliyobaki na yenyewe pia inapelekwa na kumalizia fedha zingine ili jengo hili liweze kwisha na kuondoa msongamano uliopo pale katika hospitali ya Sekou Toure?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, uzoefu unaoyesha kwamba majengo mengi yanajengwa lakini yanapokamilika, vifaa haviendi kwa wakati, watumishi hawapelekwi kwa wakati. Je, Serikali imejiwekea mpango gani mkakati kuhakikisha kwaba jengo hili litakapokamilika ifikapo 2020 basi watumishi wanapekwa, vifaa vinapelekwa ili kuweza kuokoa maisha ya mama na mtoto.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi Serikali imetenga jumla ya bilioni 30 ambazo katika hizo bilioni 30 kiasi cha bilioni 10 zinaenda kutumika kuhakikisha kwamba tunafanya ukarabati na pia bilioni 20 zinaenda kutumika kwa ajili ya kujenga hospitali za rufaa katika Mikoa ya Njombe, Geita, Simiyu, Songwe na Mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ni azma ya Serikali kuhakikisha maeneo yote yale ambayo kuna msongamano kama ilivyo hospitali ya Sekou Toure ambayo nina hakika Serikali imeanza kutoa pesa na yeye mwenyewe amekiri bilioni moja imeshatoka. Nimhakikishie kwa kadri pesa itakavyokuwa imepatikana hiyo bilioni nyingine itatoka ili ziweze kumalizia kazi iliyokusudiwa, kwa sababu lazima tuhakikishe kwamba inakamilika kwa muda tuliojipangia 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili anaulizia juu ya suala zima la kupatikana vifaa pamoja na watalaam wa kuweza kutoa huduma kama ambavyo tumetarajia. Naomba nimhakikishie yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge ni shuhuda kwamba sasa hivi Serikali imetangaza nafasi kwa ajili ya kuajiri watumishi kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, lakini pia kupitia Wizara ya Afya. Ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba watumishi wanapatikana, hilo naomba nimwondoe shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala zima la vifaa tumekuwa tukipeleka pesa moja kwa moja MSD ili pale ambapo hospitalii zinakamilika na vituo vya afya vinakamilika vifaa navyo vinapelekwa mara moja.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ukweli ni kwamba hospitali hii ya rufaa sio tu inahudumia wananchi wa Mkoa wa Mwanza, bali na wananchi wengi wa Mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu ya umuhimu huo, hospitali ya Sekou Toure ambayo kwa kweli inatoa huduma kubwa na nzuri kwa sasa, ni nini, mkakati wa Serikali kuwatumia hao hao Wakala wa Majengo (TBA) wakati wanaendelea na mikataba ikiwezekana kwa sababu wao ni Wakala wa Serikali, wawe wanatumia fedha zao za ndani kuhakikisha miradi waliyopewa inakamilika na wao wanabaki kudaiana na Serikali ili kutoa huduma kwa wananchi kwa haraka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Mwenyekiti, TBA pesa ambazo wanazipata zinatokana na project mbalimbali, sasa nadhani sio busara sana ukasema watumie pesa walizonazo ambazo zitakuwa zimetokana na project fulani ambayo labda haijajengwa, waanze kutumia wakisubiri kwamba Serikali ikipeleka pesa ndio ziende sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kadri makusanyo yanavyokwenda na yeye mwenyewe ni shuhuda, kasi yetu katika ujenzi wa vituo vya afya na hospitali za Wilaya pamoja na hospitali za rufaa hautiliwi mashaka. Naomba avute subira haya mambo yatakwenda vizuri kabisa.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kusuasua kwa ujenzi wa hospitali ya rufaa Mkoa wa Mwanza, kunafanana na kusuasua kwa ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini ambayo inajengwa Manispaa ya Mtwara. Sasa ningependa kujua Serikali ina mpango gani wa muda mfupi wa kukamilisha ujenzi wa hospitali hiyo ya rufaa Kanda ya Kusini ili ianze kutumika haraka iwezekanavyo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika jibu langu la swali la msingi kuna kiasi cha shilingi bilioni 10 ambazo zimetengwa mahususi kwa ajili ya kwenda kufanya ukarabati na kumalizia majengo ambayo tayari yalishaanzishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie na hasa baada ya kutenganisha kwamba hospitali za rufaa zinakuwa chini ya Wizara ya Afya, kasi itaongezeka tofauti na ambavyo mwanzo zote zilikuwa chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuondoa huu mzigo naamini ni rahisi sana kwa Wizara ya Afya, kusimamia na kuhakikisha kwamba hiyo hospitali ambayo ilishaanza kujengwa inakamilika kwa wakati.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa ujenzi wa kituo kile cha afya ulitokana na ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alipotembelea katika Kata zile mbili za Nalasi zilizoko katika kijiji kimoja na kuagiza kwamba kipatikane Kituo cha Afya; na kwa kuwa Halmashauri imekuwa ikipanga kila mwaka bajeti ya kujenga kituo kile kwa shilingi milioni 80 na shilingi milioni 75, lakini mpaka leo hii bado wameshindwa kujenga kituo kile. Je, Serikali haioni haja sasa ya kutimiza ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne kwa kutoa fedha kwa ajili ya kujenga kituo kile cha afya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina gari moja ambalo ni bovu tangu 2007, mpaka leo ni zaidi ya miaka 11; na kwa kuwa eneo la Tunduru ni kubwa sana, lina Majimbo mawili (Kusini na Kaskazini), je, Serikali haioni umuhimu sasa kutoa gari mbili za wagonjwa upande wa Kaskazini na Kusini ili kuweza kuhudumia wananchi wa Wilaya ya Tunduru ambao eneo lao ni zaidi ya square kilometer 18,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mpakate, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza anaulizia Serikali kutoa nguvu ili kumalizia hicho kituo cha afya. Pesa ambayo imepelekwa, shilingi milioni 400 na shilingi milioni 500 inaashiria dhamira njema ya Serikali ya kuhakikisha kwamba vituo vya afya vinajengwa hususan katika Halmashauri ya Tunduru. Halmashauri nayo ina vyanzo vyake, kwa bajeti ambayo inaisha mwaka 2017/2018 wameweza kukusanya wastani wa shilingi bilioni 2.78 na katika bajeti inayokuja, wanatarajia kukusanya shilingi bilioni 3.1, ni wazi kabisa hakika wakiweka kipaumbele cha kumalizia hicho kituo cha afya na kwa sababu wamesaidiwa na Serikali, wanaweza kumaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kuhusu kupeleka ambulance, ni kweli tangu mwaka 2007 ile gari itakuwa imeshakuwa chakavu kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi. Ni vizuri tukashirikiana na Halmashauri kwa kutumia vyanzo vyao wakati Serikali Kuu tunahangaikia, tukipata, tutakuwa tayari kuwafikiria lakini siyo vizuri nao wakabweteka kwa sababu wana chanzo kizuri na wanakusanya vizuri. Ni vizuri kiasi hicho ambacho kinapatikana wakatenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kununua ambulance, sidhani kama itaathiri sana Halmashauri. (Makofi)
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ina Vituo vya Afya vinne vya Kichiwa, Lupembe, Sovi na Matembwe. Katika vituo hivi vyote hakuna gari hata moja la wagonjwa, ni lini Serikali itatuletea gari la wagonjwa kwa ajili ya vituo hivi ukizingatia kwamba Kituo cha Lupembe tunafanya operesheni lakini hatuna gari? Inapotokea tatizo la watoto njiti, inakuwa ni shida sana kuwakimbiza Kibena, zaidi ya kilometa 80. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la ndugu yangu Mheshimiwa Hongoli, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nia njema ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma za afya zinasogezwa na hasa maeneo ambayo ni mbali kuwe na gari kwa ajili ya kusafirisha wagonjwa. Pia ni ukweli usiopingika kwamba uhitaji ni mkubwa na ndiyo maana tumekuwa tukitoa magari kwa kadri yanavyopatikana na uwezo wa kibajeti unavyoruhusu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kadri fursa itakavyopatikana, tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba kule Lupembe ambako ni mbali nako gari inapatikana.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri nyingi ikiwemo ya Tabora Manispaa uwezo sasa wa kifedha hasa zile zinazotokana na own source umepungua kutokana na baadhi ya mapato ya Halmashauri kwenda kwenye Serikali Kuu na hii imesababisha huduma nyingine kama za afya na hasa vituo vya afya Halmashauri kushindwa kupeleka fedha kule kutokana na upungufu huo. Serikali ina mpango gani wa kuziba pengo hilo ili zile Halmashauri ambazo hazina uwezo ziweze kupata fedha ambazo zinaweza kusaidia vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kutembelea Manispaa ya Tabora na katika nafasi ile tulitembelea na kuona vyanzo vya mapato vya Manispaa ya Tabora. Nilikuwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge na tukawashauri, vile vyanzo vilivyopo kwanza ni vizuri wakavisimamia wakahakikisha kwamba hakuna hata senti tano ambayo inapotea. Tulitembelea eneo la stendi, jinsi ambavyo wanakusanya hatukuridhika na jitihada ambazo zinatumika katika kukusanya, lakini pia kuna vyoo pale na maeneo mengi ambayo hakika wakisimamia vizuri, bado ni maeneo oevu ambayo pesa zinaweza zikakusanywa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kushirikiana na Halmashauri pamoja na TAMISEMI, nguvu yetu tukiweka pamoja hakika huduma katika vituo vya afya na hospitali zitaweza kuboreshwa. Naye mwenyewe ni shuhuda, ameona jinsi ambavyo bajeti ya afya imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mpaka shilingi bilioni 269. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ni azma na nia ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha vituo vya afya.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri alibahatika kufanya ziara katika Jimbo letu la Babati Mjini, nasi tukamuonesha jinsi gani tumeathirika baada ya vyanzo vyetu vya Halmashauri kuchukuliwa na Serikali Kuu. Hivi karibuni mliwaita Wakurugenzi, Wenyeviti wa Halmashauri na Maafisa Mipango mkasema kwamba mtatupatia fedha na gawio letu lilikuwa shilingi milioni 900 kwa ajili ya kukamilisha vituo hivi na miradi mingine. Naomba nifahamu, fedha hizo shilingi milioni 900 zinafika lini Babati maana Vituo vya Singe, Mutuka na Sigino tumeshapaua, tunasubiri hela za finishing?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tuliwaita Wenyeviti na Wakurugenzi ili waainishe vipaumbele katika maeneo ambayo yataenda kuanza kutumika pindi pesa itakapokuwa imepelekwa kule kwao na wakaainisha. Ofisi ya Rais, TAMISEMI zoezi lile tulishalikamilisha na tulishakabidhi Hazina. Ni matarajio yetu kwamba Hazina wakishakuwa na pesa ya kutosha kutoa, tutaweza kupeleka ili zikafanye kazi ambazo zilikusudiwa. (Makofi)
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, ni kweli Serikali imeweza kufanikiwa kujenga kituo kama alivyosema kilichogharimu shilingi milioni 400 katika Wilaya ya Mkalama, lakini Wilaya ile inahitaji vituo vingi vya afya na yapo majengo ambayo wananchi tayari wameshaanza kuyajenga na yamefikia katika kiwango cha kupaua. Je, Serikali iko tayari sasa kuja kukamilisha kituo kingine cha afya ili wananchi waweze kupata huduma bora? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika Jimbo la Singida Kaskazini tunavyo vituo viwili vya afya. Kituo cha Mgori na Kituo cha Ilongero na vituo hivi havijapata fedha za ukarabati na havifanyi upasuaji ukizingatia kwamba Halmashauri yangu haina hospitali. Je, Serikali iko tayari sasa kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha vile vituo vianze kutoa huduma ya upasuaji na wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini waweze kupata huduma? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli ambao uko dhahiri na sisi Waheshimiwa Wabunge wote ni mashuhuda jinsi ambavyo Serikali imetilia maanani suala zima la afya kwa maana ya kujenga vituo vya afya pamoja na hospitali za Wilaya pamoja na kuziboresha Hospitali za Rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu hii kasi ambayo tumeianza siyo ya nguvu za soda, tutaendelea nayo kuhakikisha kwamba tunaboresha masuala mazima ya afya ikiwemo katika Jimbo la Mkalama.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Monko ni shuhuda kwamba hivi karibuni Kituo chake cha Afya cha Mgori kimepelekewa pesa. Hii yote ni kuonesha jinsi ambavyo Serikali inajali afya za wananchi na jinsi ambavyo inaboresha huduma za afya. Naomba awe na subira kwa kushirikiana na Serikali hakika tutapiga hatua mbele zaidi.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana nami kuniruhusu niulize swali la nyongeza kwenye swali hili 496. Kwa vile Jimbo zima la Tabora Kaskazini lina kituo kimoja tu cha afya na Mheshimiwa Rais alipopita katika Jimbo langu aliambiwa tatizo hili na akachangia shilingi milioni 10 ili kujenga Kituo cha Afya pale Mwagelezi na Mbunge akachangia shilingi milioni tano. Je, Serikali iko tayari kutuongeza hela ili kituo kile kikamilike? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kwa dhati kabisa nipongeze juhudi ambazo Mheshimiwa Mbunge amekuwa akizifanya kwa kushirikiana na wananchi wake. Jana tumepokea barua yake ambayo inaonesha jinsi ambavyo amechangia kutoka Mfuko wa Jimbo na pia katika kutoka vyanzo vyake katika suala zima la kuhakikisha afya inaboreshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie, kwa jitihada na nguvu ambazo ameanzisha pamoja na wananchi wake, kwa kadri nafasi itakavyoruhusu na bajeti ikiruhusu hakika hatutasahau kuhakikisha kwamba tunapeleka huduma ya afya. Kama ambavyo amekuwa akisema kwamba siku hizi mzigo mzito humbebeshi Mnyamwezi unampunguzia unataka kila mtu abebe wa kwake, naomba nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma ya afya Uyui inaboreshwa. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kwa ajili ya kuuliza swali kwenye Wizara hii. Mheshimiwa Naibu Waziri atakumbuka wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Jimbo la Ndanda kwa maana ya Mkoa wa Mtwara alitembelea Kituo cha Afya cha Chiwale ambacho alikizindua siku ile.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote, Kituo cha Afya cha Chiwale kina uhaba mkubwa sana wa watumishi na barua tulishaipeleka toka mwezi wa Tatu kwa Waziri wa Utumishi, Mheshimiwa Mkuchika, nafikiri kwa kushirikiana na idara yake na Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema, pamoja na kufungua kituo kile cha afya mara moja atahakikisha watumishi wameletwa pale kwa ajili ya kupunguza tatizo lililoko pale. Je, ni lini sasa Wizara itapeleka hao watumishi Kituo cha Afya cha Chiwale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna suala zima la upungufu wa watumishi kwa upande wa afya na hivi karibuni Ofisi ya Rais, TAMISEMI imetangaza nafasi kwa ajili ya kuajiri watumishi wa afya ili kujaribu kupunguza pengo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mchakato uko kwenye hatua za mwisho kabisa, haitapita mwezi kazi hii itakuwa imeshakamilika. Namwomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika maeneo ambayo kuna upungufu mkubwa tutazingatia kuhakikisha kwamba watumishi wanapalekwa ikiwa ni pamoja na kituo chake cha afya.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Iramba ina changamoto kubwa hususani kwa watumishi na vifaatiba. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka haraka watumishi na wataalam katika afya ya uzazi wa mpango? Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla wake Mkoa wa Singida wamekuwa wakipigania suala zima la afya na jana nimejibu swali la Mheshimiwa Mbunge huyu ambaye leo ameuliza swali la nyongeza. Naomba nimhakikishie, kama nilivyotoa majibu alivyouliza Mheshimiwa Mwambe, mchakato wa ajira uko kwenye hatua za mwisho na lengo ni kuhakikisha kwamba maeneo yale yote ambayo yana upungufu yanapelekewa watumishi. Naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, zoezi likikamilika tutapeleka watumishi wa upande wa afya ili kupunguza hizo changamoto.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Miaka mitatu mfululizo iliyopita Madaktari wamekuwa wakihitimu vyuo vyetu vikuu vya humu ndani. Madaktati wako wanasubiri ajira na sekta ya afya ina upungufu wa zaidi ya asilimia 50 ya Madaktari katika vituo mbalimbali na sekta nzima. Je, kwa nini Serikali isi-fast truck ili Madaktari hawa walioko mitaani wakaingia kwenye utumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba tuna uhitaji mkubwa wa Madaktari, lakini pia atakubaliana na mimi kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI imetangaza nafasi na kama hilo halitoshi na Wizara ya Afya nayo imetangaza nafasi kwa ajili ya hao Madaktari na Wauguzi kwa ujumla wake. Naomba nimhakikishie kwamba mchakato upo pazuri, kwa hiyo, hicho ambacho anaulizia kuhusiana na suala zima la ku-fast truck ingekuwa tumechelewa wakati ule lakini kwa sasa hivi tuko hatua za mwisho, naomba avute subira hili litakamilika.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali ambayo kimsingi yameacha kujibu kipengele (b), sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Lusewa ni Mji Mdogo ambao sasa hivi umeshapandishwa hadhi na kuwa Mji Mdogo. Ni eneo ambalo lina wakazi wengi sana. Kutoka Lusewa kwenda Nalasi kuna umbali wa kilometa 150 na kutoka Lusewa kwenda Songea Mjini kwenye hospitali ya rufaa kuna kilometa 150. Wanawake wenzangu wa eneo hilo la Lusewa katika Mji Mdogo wamekuwa wakipata shida sana hasa kwenye suala la usalama wao wa uzazi na usalama wa mama na mtoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, wanawake na watoto wamekuwa wakipoteza maisha na siku moja nilisimama hapa katika Bunge lako Tukufu nilionesha hisia zangu kwamba imefika mahali sasa kumtoa mwanamke kwenye Kituo hiki cha Lusewa ambacho hakina theatre kumpeleka Nalasi kilometa 150, gari la kubebea hao wagonjwa hakuna, wakati mwingine ni mabovu. Naomba Serikali inipe majibu ya kina ni lini itakamilisha ujenzi wa kituo hiki cha afya pamoja na kuweka hii theatre ambayo itawasaidia akinamama hawa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, anyway siyo swali lakini ni ombi, niseme kwamba, je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuongozana nami pamoja na Mbunge wa Jimbo la Namtumbo, Mkurugenzi wa Namtumbo na DMO wa Namtumbo ili aende akaone mwenyewe kwa macho jinsi ambavyo wanawake wanavyopata tabu na watoto wanapoteza maisha katika maeneo yale? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi kwamba ujenzi wa kituo kile cha afya umekamilika isipokuwa chumba cha upasuaji kilichobaki ni sakafu peke yake. Naomba nitumie fursa hii kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ahakikishe kwamba katika vyanzo vyake vya mapato kwa kushirikiana na wananchi kazi ya kumalizia sakafu iweze kukamilika ili wananchi waendelee kupata huduma badala ya kusubiri mpaka hicho kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Naamini kabisa katika vyanzo vyao vya mapato wakijibana wanaweza kumalizia kabisa suala zima la sakafu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameomba mimi kuambatana na Waheshimiwa Wabunge wa maeneo hayo. Naomba nimhakikishie, katika maeneo ambayo nina deni la kwenda kujionea mimi mwenyewe ni pamoja na Mkoa wa Mtwara lakini nikitoka Mtwara nitakuwa naenda Ruvuma halafu nitakwenda Njombe. Ilikuwa niende kwa bahati mbaya nikawa nimepatwa na msiba. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ahadi ni deni na kwa vyovyote vile Ilani hutekelezwa ndani ya miaka mitano, imekuwa ni kawaida kwamba Ilani ya Chama cha Mapinduzi mara nyingi haitekelezwi siyo tu kwenye masuala ya afya ni pamoja na barabara na elimu. Nataka kupata kauli ya Serikali, je, hizi ahadi zao hasa za Marais zinakuwa ni za kuwadanganya watu? Pia ni lini sasa ahadi zote kuanzia zile za Mheshimiwa Mkapa…
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili ambalo linaulizwa leo halina tofauti kabisa na ambalo aliuliza Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kuhusiana na ahadi za wagombea Urais na utekelezaji wa Ilani ya CCM. Katika majibu yangu ambayo nilitoa siku ile nilieleza kwamba ahadi zimekuwa zikitekelezwa na Waheshimiwa Wabunge wengi wamekuwa wakishukuru jinsi ambavyo ahadi zinatekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ahadi za wagombea Urais ndiyo mkataba wao na wananchi na wananchi wamekuwa wakiwapigia kura kwa ku-base kwenye hizo ahadi ambazo zinatolewa na Ilani ya CCM inatekelezwa ndani ya miaka mitano.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru kwa sababu amekuwa anafuatilia utekelezaji wa Ilani ya CCM na yeye mwenyewe anaamini kwamba tunatekeleza. Sasa amesema haitekelezwi, nadhani hapo atakuwa amepitiwa. Akatazame yale tuliyoahidi mangapi tumetekeleza, suala zima la afya yeye mwenyewe ni shuhuda na juzi tulikuwa tunaongea naye kuhusiana na barabara ya kule kwake na kazi imeshaanza kufanyika, kwa hiyo tunatekeleza. (Makofi)
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza; Kituo cha Afya Kibiti kimezidiwa, je, ni lini Serikali itafanya ukarabati mkubwa ikizingatia pale hakuna X-ray, nyumba za wagonjwa na maabara ya uhakika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ungando, Mwenyekiti wa Wandengereko ambaye kwa mara ya kwanza amenipandisha boti nikaenda Delta, sehemu ambayo unaambiwa kwamba ikifika muda fulani maji yakikauka inabidi usibiri saa nne. Nimefika kule na naomba nimpongeze jinsi ambavyo anapigania wananchi wa Jimbo lake la Kibiti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri kazi ambayo tulienda kusimamia sasa inakwenda vizuri. Kuna mambo ya hovyo yalikuwa yanafanyika katika ujenzi wa kituo kile cha afya lakini hata jana nilikuwa naongea na Mwenyekiti wa CCM ambaye alikuwa Mbunge, Ndugu Jabir Marombwa amenihakikishia ujenzi unakwenda vizuri. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, eneo hilo ambalo hakuna X-ray tayari tumeshapeleka pesa MSD kwa ajili ya vifaa, kwa sababu tunataka vituo vya afya vikamilike kwa kuwa na vifaa pamoja na wataalam ili vitoe huduma iliyokusudiwa kwa wananchi. (Makofi)
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na upungufu wa watumishi katika sekta ya afya lakini maslahi ya watumishi katika sekta ya afya yamekuwa duni hasa on call allowance ambayo Serikali kwa muda mrefu sasa haijapeleka fedha hizo katika OC. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo ili kusaidia Madaktari kufanya kazi zao kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, hivi leo ninavyoongea katika maeneo yote ambayo kumekuwa na hamasa kubwa wananchi wakajiunga na CHF, hakuna tatizo la Madaktari kulipwa on call allowance. Akitaka kuchukua mfano, nimeenda Tanga pale sasa hivi katika hizi pesa ambazo wananchi wanachangia kwa kujiunga na Bima ya Afya, kulipana on call allowance si tatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba Mheshimiwa Mbunge ahamasishe maeneo ya kwake wananchi wajiunge na Bima ya Afya na michango ile ambayo inatolewa ya ‘Papo kwa Papo, Tele kwa Tele’ hakika katika maeneo yote ambayo nimepita tangu utaratibu huu umeanza, kulipana on call allowance siyo tatizo tena.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, Wilaya ya Mbogwe pamoja na Mikoa ya Kanda ya Ziwa tuna matatizo makubwa sana ya huduma za afya, matokeo yake wananchi walio wengi wanategemea sana huduma za waganga wa jadi na huko wakati mwingine wanapata uchonganishi na kuuana. Je, Serikali itakuwa tayari sasa kuwajengea wananchi wa Mbogwe Hospitali yao ya Wilaya? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, pamoja na kuipongeza Serikali kutupatia shilingi milioni 800 kwa ajili ya vituo vya Afya vya Iboya na Masumbwe. Je, Serikali iko tayari sasa kutupatia wataalam zaidi pamoja na vifaatiba? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba Mikoa ya Kanda ya Ziwa pale ambapo huduma ya hospitali inakosekana wamekuwa wakitumia tiba mbadala na kwa Mheshimiwa Mbunge imekuwa ni jambo la kawaida. Hata hivyo, sasa hivi tangu Serikali kwa kushirikiana na wananchi wameanza zimeanza kujengwa zahanati pamoja na vituo vya afya, naamini mentality imeenda iki-change.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilienda Jimbo la Itilima kwa Mheshimiwa Silanga nikakuta kuna zahanati nyingi sana ambazo zimejengwa kwa kushirikisha wananchi na mwitikio ni mkubwa sana. Naomba hiyo kazi nzuri ambayo wameanza wenzetu wa kule ni vizuri na Mheshimiwa Mbogwe na yeye akaiga mfano mzuri ili wananchi wetu wahame katika tiba mbadala ambayo imekuwa ikisababisha mpaka watu kuuana kwa sababu ya masuala mazima ya kupiga ramli.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili juu ya suala zima la kupeleka wataalam, naomba nimhakikishie kwamba baada ya mchakato kukamilika wameajiriwa wataalam hakika na yeye mwenyewe anakiri kwamba tumempelekea vituo viwili vya afya. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba na wataalam wanapelekwa ili vituo vya afya vifanye kazi iliyokusudiwa.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tatizo la Hospitali ya Wilaya lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe ni sawa na tatizo la Hospitali ya Wilaya katika Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Tayari Hospitali ya Mawenzi imezidiwa na wagonjwa kama Hospitali ya Mkoa na Manispaa ya Moshi kwa muda mrefu imekuwa na ombi hilo la Hospitali ya Wilaya ambalo tayari Serikali imeonekana imelikubali. Je, ni lini Serikali sasa italeta fedha ili hiyo Hospitali ya Wilaya ya Manispaa ya Moshi iweze kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo ambayo Hospitali za Wilaya hazipo zinaenda kujengwa na ndiyo maana tumeanza na hospitali 67. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya kwamba hizo 67 kukamilika hatutaishia hapo tutaenda maeneo mengine ambayo hakuna Hospitali za Wilaya ili tuweze kujenga.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika juhudi za kuboresha huduma za afya katika Jimbo la Bagamoyo, wananchi katika Kata mbalimbali zikiwemo Nianjema, Fukayosi na Mapinga wameanza ujenzi wa zahanati katika vijiji vyao. Je, nini kauli ya Serikali kuhusu kuwaunga mkono kumalizia ujenzi wa zahanati hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu naomba kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Shukuru Kawambwa maana katika vituo vya afya vilivyojengwa vya kupigiwa mfano ni pamoja na Kituo chake cha Afya cha Bagamoyo. Naomba na wengine wa mikoa ya jirani ambao vituo vya afya vinaendelea kujengwa wakatazame mfano mzuri jinsi ambavyo walivyosimamia na value for money ikaonekana katika Kituo cha Afya cha Bagamoyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama ambavyo Serikali imekuwa ikiwaunga mkono maeneo mengine katika Jimbo lake, tukimaliza hatua hii, kama ilivyo kwenye Ilani ya CCM kwamba tunahakikisha tunajenga zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata, naomba tuvute subira hicho ndicho ambacho ni ahadi yetu sisi kwa wananchi, tutaenda kutekeleza.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuulizwa swali la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali nyingi za Wilaya kama Hospitali ya Sinza, Dar es Salaam ambayo ilikuwa Kituo cha Afya cha Sinza Palestina kimepandishwa hadhi na kuwa Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo, hospitali hiyo haipati fedha kama Hospitali ya Wilaya na kukosekana kwa fedha hizo kumesababisha hospitali kushindwa kukidhi mahitaji yake ikiwemo kuwa na chumba cha kuhifadhia maiti. Je, Serikali iko tayari kupeleka fedha za Hospitali ya Wilaya katika Hospitali ya Sinza Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kukumbusha kwamba swali hili limekuwa likiulizwa la Sinza Palestina, naomba nimjibu Mheshimiwa Said Kubenea kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nilishawahi kujibu hapa, Kituo cha Afya cha Sinza Palestina siyo Hospitali ya Wilaya. Katika jibu langu ambalo nililitoa siku ile nilitaka Halmashauri wahakikishe kwamba wanatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Nikajibu pia kwamba katika kituo cha afya na hii ni changamoto katika vituo vya afya vingi ambavyo viko mijini tunakosa jina hasa ambalo tungeweza kusema kwa sababu viko juu ya vituo vya afya vya Kata za vijijini lakini pia havifikii hadhi ya Hospitali ya Wilaya. Ndiyo maana ukienda Sinza Palestina pale tumepeleka mpaka Madaktari Bingwa lakini bado hiyo haitoi mwanya kwamba tuseme ni Hospitali ya Wilaya. Kwa sababu Hospitali ya Wilaya inahitaji eneo la ukubwa usiopungua ekari 25.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulishawaambia Halmashauri yake watenge eneo hilo ili tujenge Hospitali ya Wilaya kama ambavyo tunafanya kule Kivule kwa Mheshimiwa Waitara ili tuwe na hospitali za Wilaya kupunguza msongamano katika hospitali zingine.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa Halmashauri ya Morogoro mpaka sasa haina hospitali ya Wilaya na kwa kuwa Tarafa ya Ngerengere na mahali ambapo panajengwa hospitali ya Wilaya kuna umbali wa zaidi ya kilometa 105.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Ngerengere kuna miradi mitatu mikubwa ya Kitaifa ambayo ni standard gauge pamoja na ujenzi wa kiwanda cha sukari pamoja na Bwawa la Kidunda ambao unasababisha wingi mkubwa wa watu. Je, Serikali haioni umuhimu wa kukarabati Kituo cha Afya Ngerengere ili kiwe na hadhi ya kituo cha afya kuweze kuwa-accommodate watu hawa wote na kujenga Kituo kingine cha Afya katika Kata ya Mkulazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabla ya kujibu naomba nitangulize maneno yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo tumekuwa tunapata taabu pale ambapo pesa za maendeleo zinapelekwa hazifanyiwi kazi kwa wakati ni pamoja na kwa Mkurugenzi wa Halmashauri anayotoka Mheshimiwa. Kuna pesa zimepelekwa kwa ajili ya kujenga kituo cha afya lakini kasi yake ni mbovu sana. Naomba nichukue fursa hii kwanza kumuagiza Mkurugenzi ahakikishe kwamba pesa iliyopelekwa inatumika kukamilisha ujenzi wa kituo cha afya ili wananchi waweze kupata huduma ya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha maeneo yale yote ambayo iko haja na kama ambavyo ametaja umbali na ni ukweli usiopingika kwamba Ngerengere ina umuhimu wake. Naomba nimhakikishie kwamba baada ya hili zoezi kukamilika na mimi nikapata fursa ya kwenda, tutashauriana namna nzuri ya kuweza kuhakikisha ukarabati unafanyika na huko.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Napenda kuipongeza Serikali kwa kutenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nyang’hwale. Napenda niiulize Serikali, huduma ya X-ray kwa Wilaya ya Nyang’hwale ni shida sana. Kuna ajali mbalimbali ambazo zinatokea na kuifuata huduma ya X-ray karibu kilomita 110. Je Serikali ina mpango gani wa kuleta mashine ya X-ray katika Hospitali ya Wilaya ya Nyang’hwale? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wamefanya vizuri kwenye suala zima la afya kwa maana ya ujenzi wa vituo vya afya na zahanati ni pamoja na kwa Mheshimiwa Amar. Naomba nimpongeze kwa dhati kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba X-ray zinakuwepo ndani ya vituo vyote vya afya na ndiyo maana katika maboresho ambayo yamefanyika hivi karibuni ni pamoja na kuongeza jengo la X-ray. Sasa kama X-ray zinakuwepo kwenye vituo vya afya sembuse hospitali ya wilaya! Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tukitoka hapa tuwasiliane tujue nini hasa ambacho kimetokea mpaka hospitali yake ya Wilaya ikose X-ray. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wananchi wamekuwa wakishiriki huduma za afya kwa kujenga maboma. Kwenye Kata yangu ya Kimuri, wananchi wameweza kujenga vyumba zaidi ya 20 lakini vyumba hivi vimekaa zaidi ya miaka 10 Serikali haijaweza kukamilisha. Je, Mheshimiwa Waziri wako tayari kukamilisha hivyo vyumba ili wananchi waweze kupatiwa huduma bora ya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo Serikali tunaenda kujenga vituo vya afya pamoja na hospitali za Wilaya ni pamoja na Mkoa wa Kagera. Naamini Mheshimiwa Mbunge naye ni miongoni mwa Waheshimiwa Wabunge wanufaika katika Serikali ya Awamu ya Tano ambao wanaenda kupata huduma hii ambayo haikuwepo kwa muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la kukamilisha hivyo vyumba 20 ambavyo anavisema, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, wanasema kuona ni kusadiki. Ni vizuri pale ambapo tutapata nafasi ya kwenda kutazama ili tujue uhalisia na bajeti kiasi gani itahitajika kumalizia huo ujenzi ili nguvu ya wananchi isije ikapotea, kama Serikali tutakuwa tupo tayari.
MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, amenitendea haki. Kwa kweli katika mwaka huu, leo nina furaha kubwa sana, kwanza Serikali imenipatia shilingi milioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali mpya ya Wilaya ya Songwe, nimefarijika sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mwanzo wa mwezi huu alikuja Dkt. Kalindu kutoka Hospitali ya Mwambani kuleta tatizo hili kwa ajili ya kuteuliwa Hospitali Teule ya Wilaya. Kwa hiyo, Serikali leo imejibu kwamba imepandisha hadhi na mkataba wetu umekubaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja tu la nyongeza. Kwa vile sasa imekubaliwa kuwa hospitali ya wilaya, naomba kujua ni lini kibali kitatoka, maana ndiyo imekuwa hospitali ya wilaya lakini watumishi pale ni wachache na tangu mwaka 2014/2015 hatujawahi kupata vibali vya watumishi. Naomba nijue ni lini Serikali itatoa kibali cha kuajiri watumishi (madaktari na wauguzi) katika Hospitali ya Mwambani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mwalimu Mulugo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu, naomba uniruhusu nimpongeze sana Mheshimiwa Mulugo kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia suala hili. Alikuja Daktari kutoka Hospitali ya Mwambani lakini pia na juzi imekuja Kamati ya Siasa ya Wilaya yake nao wakawa wanaulizia suala hili. Kama ambavyo nilimuahidi tutafanya mapema na hili limewezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake anataka uhakika juu ya suala zima la kupata watumishi. Naomba nimhakikishie process ya ajira iko kwenye hatua za mwisho kabisa, zaidi ya wiki mbili tayari tutakuwa tushakamilisha suala la ajira na hakika tutahakikisha tunapeleka watumishi ili wakafanye kazi kwenye ile hospitali ambayo tumekubali itumike kama Hospitali ya Wilaya kwa sasa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi pamoja na majibu ya Serikali, naomba nieleze kwamba gari lililopo Kituo cha Afya Kala ni bovu sana na halifanyi kazi na Kala ipo umbali wa kilometa 150; hakuna mawasiliano yoyote ya simu wala barabara haifai. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza kwenye huduma za afya zinazotolewa kwenye vituo vyenye udau wa Serikali na wadau wengine, wananchi wa Kala wameamua kujenga kituo cha afya kwenye Kijiji cha King’ombe wao wenyewe, lakini vilevile wako wananchi wengine wameamua kujenga kutoka kwenye kata zao, Kata ya Ninde, Kata Kate na Kata ya Nkandasi. Je, Serikali iko tayari kuunga mkono juhudi hizi za wananchi?
Swali la pili Waziri wa Afya alipotembelea kwetu alituahidi kutupata shilingi milioni 400 kwenye Kituo cha Afya cha Wampembe na mpaka sasa sijaona fedha hiyo zimeonekana katika vitabu mbalimbali, lakini pia hatujazipokea; je, Serikali bado ina mpango huo wa kutupatia pesa katika Kituo hicho cha Wampembe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nichukue fursa hii kuwapongeza wananchi kwa dhati kwa moyo wao wa kujitoa kuhakikisha kwamba vinajengwa vituo vya afya baada ya kuona kwamba changamoto ya kuwa katika hivi vya ubia inawakabili. Katika Serikali kuunga jitihada za wananchi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika pesa ambayo inatarajiwa kupatikana muda si mrefu Kituo cha Afya Kasu nacho ni miongozi mwa vituo vya afya ambavyo vinaenda kupatiwa fedha ili viweze kujengwa na kuweza kutoa huduma ambazo wananchi wanatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili ameniambia kwamba Mheshimiwa Waziri wa Afya alivyoenda baada ya kuona changamoto kwa wananchi wa Wampembe aliahidi kituo hicho kingeweza kupatiwa jumla ya shilingi milioni 400 ili kiweze kupanuliwa. Naomba nimhakikishie kwamba ahadi hiyo bado ni thabiti ni suala la tu la muda, pesa ikipatikana hatutasahau.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa ujumla wake naomba uniruhusu, unajua unapokuwa na Waheshimiwa Wabunge ambao wako kwenye Halmashauri moja na majimbo yako mawili ni sawa na ambavyo unapokuwa na watoto mapacha. Ni wajibu wako kuhakikisha kwamba unakuwa na balancing ambalo kama Serikali tunaenda kulifanya. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetoa waraka wa kusitisha taratibu wa upandishwaji wa baadhi ya zahanati kwenda vituo vituo vya afya ikitaka vituo vya afya vijengwe kwenye kila kata, lakini kwamba Halmashauri zetu hazina fedha za uhakika za kujenga lakini hata wananchi wenyewe hali ya uchumi ni ngumu kuweza kujenga vituo hivyo vya afya.
Je, Serikali kwa nini msifikirie kwa upya kubatilisha uamuzi huo na kuangalia zile zahanati ambazo kwa kweli zinakidhi haja ziweze kupandishwa kuwa vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya suala zima la kupandisha zahanati kuwa vituo vya afya, kwanza naomba tukubaliane, zahanati zina ramani zake na vituo vya afya vina ramani zake. Hoja ya msingi ni kwamba tungependa wananchi wapate huduma ya afya jirani sana, naomba kwa sababu mpaka sasa hivi tulikuwa tunaongelea tuna asilimia 12 tu ya vituo vya afya na bado na uhitaji wa zahanati bado uhitaji ni mkubwa.
Naomba azma hiyo ya Serikali yakuhakikisha kwamba kila kijiji kinakuwa na zahanati na kila Kata kunakuwa na kituo cha afya bado ndio msimamo wa Serikali na wananchi waendelee kushiriki ili tuhakikishe kwamba huduma hii ina inawasogelea wananchi kwa karibu.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, tatizo hili la wanawake wajawazito waliojifungua ku-share vitanda lipo pia kwenye Hospitali ya Wilaya ya Arumeru na mimi nikishirikiana na DMO aliyekuwepokwa sababu ya PR tulipata wafadhili ambao walikuwa tayari kutujengea maternity ward kubwa na nzuri na kisasa kabisa kwa kushirikiana na mimi na Dkt. Okiyoo ambaye alikuwa DMO wa kwetu. Unfortunately kwa sababu binafsi ambazo siko tayari kuzitaja hapa tumeshazijadili pia na Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Mkurugenzi aliyekuwepo akafanya yake wakamhamisha DMO kumpeleka Lindi.
Baada ya kupitia na kwenda kupitia zile parameters hapo Wizarani TAMISEMI tukagundua kwamba aliondolewa kwa sababu binafsi na bahati ambaya wale wafadhili ambao walikuwa watujengee ile maternity ward ilitokana na mahusiano binafsi ambayo tulikuwepo sisi na wao na yule daktari. Kwa hiyo, baada ya yeye kuondoka ni kama wameingia mitini vile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda kuuliza tu Serikali iko tayari kumrudisha yule bwana ili ule mradi ukamilike halafu baada ya hapo wamhamishe? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali si mtu, kama alikuwa DMO pale ame-coordinate pale kwamba maternity ijengwe pale suala la yeye kuhama haiwezi ikawa kigezo cha kwamba mchakato huo usiendelee ni vizuri akarithisha hiyo kazi nzuri ambayo aliyokuwa ameishainza ili DMO aliyepo sasa afanye kuhakikisha kwamba hilo linakamilika.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Vifaa tiba ni tatizo kubwa kwenye hospitali nyingi nchini na utajiri mkubwa tulionao kuliko wote ni afya za mwanadamu.
Mheshimiwa Spika, swali, Wizara hii ina upungufu wa zaidi ya sekta ya afya zaidi ya asilimia 50 ya watumishi. Serikali inaji-commit nini kuhusu kuhakikisha watumishi wa kutosha wa Hospitali ya Newala wanapatikana kwa wakati ili waweze kutoa huduma zinazostahiki?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Hospitali ya Kilema iliyoko Vunjo au ya Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ina tatizo la vifaa tiba na watumishi wake kwa wakati huu nesi mmoja anahudumia zaidi ya watu 30 wodini. Serikali inatoa kauli gani hapa ili hospitali hii nayo ipate watumishi wa kutosha pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya afya za binadamu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kuhusiana na commitment ya Serikali ili kuhakikisha kwamba watumishi wa afya wanapelekwa wa kutosha Newala ni kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi. Maombi yao ni kupatiwa watumishi 60 na hii naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbatia kwa niaba ya Mheshimiwa Ajali Akbar kwamba ni commitment ya Serikali kuhakikisha pindi fursa za ajira zitakapokuwa zimetolewa hatutaisahau Newala.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Hospitali yake ya Kilema ambayo anasema wastani Nesi mmoja anahudumu wagonjwa 30 ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaweka vifaa vya kutosha lakini pia na watumishi wa kutosha. Ndio maana wakati Mheshimiwa Waziri wa dhamana ya ajira alivyokuwa anahitimisha alisema ndani ya Bunge hili tunategemea kuajiri watumishi wa kutosha. Katika watumishi 59,000 watakaoajiriwa sehemu kubwa ni upande wa elimu na afya, naomba nimuhakikishie ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunapunguza mzigo mkubwa kwa wahudumu kwa maana ya manesi ili na wao wawe na fursa ya kuweza kuhudumia wagonjwa kwa uzuri zaidi.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie na Hospitali ya Kilema tutaikumbuka.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.
Katika sekta iliyoathirika sana wakati wa zoezi la uhakiki wa vyeti, suala zima la vyeti fake ni sekta ya afya. Jimboni Mtama baadhi ya zahanati tumelazimika kuzifunga kabisa kwa sababu watu wameondolewa.
Mheshimiwa Spika, sasa kwa nini Serikali isichukue hatua za dharura kwenye haya maeneo ambayo zahanati zimefungwa badala ya kusubiri process hii ya kuajiri watumishi wapya wa afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, katika maeneo ambayo nilifanikiwa kupita na kuona kazi nzuri ambayo imefanyika katika suala zima la ujenzi wa vituo vya afya ni pamoja na Jimbo lake la Mtama, kwanza naomba nimpongeze.
Mheshimiwa Spika, tukiwa hapa ndani bungeni Mheshimiwa Mkuchika alitoa taarifa kwamba kama yuko Mbunge yeyote, wa eneo lolote ambalo tumelazimika kufunga zahanati au kituo cha afya kwa sababu ya ukosefu wa watoa huduma aandike barua ampelekee ili tatizo hili lisiweze kutokea.
Mheshimiwa Spika, naomba kama Mheshimiwa Mbunge hakuwepo siku hiyo atumie fursa na bahati nzuri yeye yuko jirani sana na Mheshimiwa Mkuchika ili hicho anachokisema kisiweze kutokea.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada kubwa za Serikali kupitia Wizara yake ya TAMISEMI kuhakikisha inaboresha vituo vingi vya afya kikiwemo na Kituo cha Afya hiki cha Ukerewe, kama Mheshimiwa Waziri anavyofahamu kwamba kumekuwa na changamoto kubwa ya watumishi, vifaa tiba ambavyo kwa kweli vingesaidia zaidi ufanisi na ubora wa utumishi kwenye hospitali hii. Je, ni lini hasa Serikali itahakikisha suala hili linafanyiwa kazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali dogo la pili, kwa sababu matatizo ya Ukerewe kwa namna fulani yanafafana sana matatizo yaliyoko kwenye hospitali ya Wilaya ya Nyamagana. Ni nini sasa mpango wa Serikali kwa sababu mara kadhaa hospitali ya Wilaya ya Nyamagana imeshaomba kupatiwa vifaa kama ultra sound na ni lini sasa Serikali inaweza kuhakikisha hospitali ya Nyamagana inapata ultra sound pamoja na X-Ray machine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, anauliza kuhusiana na Kituo cha Afya Nakutunguru kukamilika na hasa kuwepo na vifaa vya kutolea huduma, pamoja na suala zima la watumishi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vya afya vyote vinavyokamilika ni pamoja na kuwa na vifaa vya kufanyia kazi ikiwepo X-Ray, ultra sound hayo yote ni muhimu ili kituo cha afya kiweze kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaulizia hospitali yake ya Wilaya. Kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mabula amekuwa akipigania hospitali hii kwa muda mrefu kuhakikisha kwamba inatoa huduma kwa kadri inavyokusudiwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za Wilaya zinakuwa na vifaa vya kutosha ili viweze kutoa huduma inayotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni azma yetu kuhakikisha kwamba hospitali ya Nyamagana ni miongoni mwa hospitali za Wilaya ambazo zitakua kwa viwango vinavyotakiwa ikiwa ni pamoja na kuwa vifaa vyote vinavyotosheleza.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza, naishukuru sana Serikali kwa kuweza kunipatia fedha za Kituo cha Afya cha Mwese na Kituo cha Afya cha Mishamo. Tatizo ambalo lipo kwenye eneo la Wilaya ya Tanganyika vituo vya afya havina Wahudumu na Madaktari kwa ujumla. Je, ni lini Serikali itapeleka Madaktari ili waweze kufanya kazi iliyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kakoso anafahamu kabisa kwamba sasa hivi Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeshatangaza nafasi kwa ajili ya watu wa afya wakiwepo Madaktari, Wahudumu, Manesi. Naomba nimhakikishie katika hawa ambao watakuwa wameajiriwa na naamini kwamba na wengi watakuwa wameomba wakiwa wanatokea maeneo huko ili pale wanapopewa nafasi ya kwenda kufanya kazi wasije wakasema mazingira yale kwao ni mageni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha Watumishi tunawasambaza ili wakatoe huduma kwa wananchi.
MHE. RASHID A SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Lushoto na hospitali ya Wilaya ya Lushoto inahudumia Majimbo matatu na Halmashauri mbili kwa maana ya Lushoto na Bumbuli na inakabiliwa na msongamo mkubwa sana wa wagonjwa. Je ni lini sasa Serikali itaipa fedha ili kupanua huduma hizi za afya katika Wilaya ya Lushoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Wilaya ambayo Mheshimiwa Mbunge anaitaja ina population kubwa. Pia ni ukweli usiopinga kwamba Halmashauri wanajua uhitaji, naomba kwa kushirikiana na Halmashauri na hasa Mheshimiwa Mbunge akiwa wa kwanza kuelekeza namna iliyo bora ya kuhakikisha maeneo mengi vituo vya afya vinajengwa hasa kwa kushirikisha wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni vizuri kama ni suala la ujenzi wa vituo vingine ili kuweza kutoa nafasi kwa hospitali ya Wilaya, wazo hilo jema ni vizuri likaanza kwao na sisi Serikali tutaunga mkono jitihada za wananchi.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza Swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro Mkoa wa Arusha hususani Loliondo wamekuwa wakitegemea hospitali ya Waso kwenye matibabu na hali hii inapelekea msongamano mkubwa katika hospitali ya Waso. Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kujenga hospitali ya Wilaya ya Ngorongoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Magige ni shuhuda kwamba tumeweza kujenga hospitali ya Wilaya Arusha pale na Vituo vya Afya vingi ikiwepo na Murieti na yeye ni miongoni mwa watu ambao wamekuwa wakipigania suala zima la afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie tumeanza na hospitali 67, tukishamaliza hizo 67 tutaenda maeneo yale ambayo hakuna hospitali za Wilaya ili kupunguza mlundikano kwa wananchi kupata huduma.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana taarifa kwamba mchakato huu wa kuomba Mji wa Bukene upandishwe hadhi ulianza siku nyingi na mpaka Wizara ikatoa GN Namba 176 ya mwaka 1996 ambayo mpaka sasa haijafanyiwa mchakato wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwenye swali langu la msingi niliuliza, je, muundo wa kuwa na Kata moja inayoundwa na Kijiji kimoja tu ni sahihi? Kwa sabbau muundo huu unapelekea Mtendaji wa Kijiji kutokuwa na tofauti yoyote na Mtendaji wa Kata na Serikali ya Kijiji haina tofauti yoyote na WDC na ni sawa sawa na kuwa na Mkoa mmoja unaoundwa na Wilaya moja tu ambayo kutakuwa hakuna tofauti yoyote ya Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa, kwa sababu mkoa ni mmoja na Wilaya ni mmoja. Je, muundo huu ni sahihi kuwa na Kata moja ambayo inaundwa na Kijiji kimoja tu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza ananiuliza kama najua kwamba kuna GN ambayo ilikuwa imetolewa na kwamba mpaka sasa hivi GN hiyo haijafanyiwa marekebisho yoyote, taarifa hiyo ninayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, anauliza uwezekano wa Kijiji hicho kimoja kikawa Kata, naomba nitoe ufafanuzi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Selemani Zedi anajua kwamba ilikuwa mchakato wa kupandisha Kijiji cha Bukene kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo na Bukene kama ilivyo ina vitongoji vyake 11 na lengo lilikuwa hivyo Vitongoji vije vibadilike kuwa Mitaa ambayo ingeweza kutosha katika kubadilisha sasa kuwa na Mamlaka ya Mji Mdogo wa Bukene. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Selemani Zedi, taratibu hizo zingine ziendelee ili ukifika wakati ambapo Serikali itakuwa tayari kuongeza maeneo ya kiutawala na Bukene iwe na sifa ya kuweza kuongezeka.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kijiji cha Ndwamughanga kilichopo katika Jimbo la Singida Kaskazini kina vitongoji ambavyo vipo Mukulu ambavyo viko kilomita 23 kutoka Makao Makuu ya Kijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiomba Vitongoji hivi visajiliwe kama Kijiji kwa muda mrefu. Je, ni lini Vijiji hivi vya Mukulu vinaweza kupata usajili wa kuwa kijiji kinachojitegemea ukizingatia umbali ili wananchi waweze kupata huduma za Kiserikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema kuna Kitongoji ambacho kipo kilomita 20 kutoka katika Kijiji ambacho ndiyo kimezaa hicho Kitongoji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sifa za Kitongoji kutoka katika Kitongoji kuwa Kijiji sasa sina uhakika na sifa ya hicho Kitongoji ambacho kinalazimika kufuata huduma ya kilomita 20. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuzingatia vigezo na sifa za kitongoji kubadilika kuwa kijiji pindi zitakapokuwa zimekamilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI haitasita kuhakikisha kwamba Kitongoji hicho kinakuwa Kijiji kama sifa stahiki zinakidhi.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Nachingwea ina jumla ya Kata 36 na tayari inakidhi vigezo vya kupata Majimbo mawili ya uchaguzi na taratibu zote tumeshazifuata. Ni lini Wizara ya TAMISEMI itakwenda kuligawanya Jimbo la Nachingwea ili liwe na Majimbo mawili ya uchaguzi? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kwenda Wilaya ya Nachingwea na Jimbo la Nachingwea, kwa hiyo najua ambacho Mheshimiwa Mbunge anaongelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo taratibu ambazo zinatakiwa zifuatwe ili Jimbo ligawanywe na hii huwa inapelekwa kwenye Tume ya Uchaguzi ndiyo wenye mamlaka ya kugawanya Majimbo na siyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu. Labda niseme tu kweli tunaishukuru Serikali kupata, nitumie lugha ya haka kagari, tumepata gari aina ya Suzuki Maruti ndogo sana ambayo kwa mazingira ya Jimbo la Kondoa lina uwezo wa kufanya shunting katika kata tatu za mjini tu, huku pembezoni litakuwa haliwezi kwenda kabisa kwa sababu njia haziruhusu. Je, ule umuhimu wa uhitaji wa huduma hii, Serikali haioni?.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; barabara kubwa imekamilika ya kutoka Dodoma kwenda Babati. Ongezeko la uhitaji wa huduma za dharura umekuwa mkubwa kweli, ajali ni nyingi kila uchao tunapata taarifa hizi, gari hili haliwezi kumudu. Je, ni lini sasa Serikali itatuletea gari la wagonjwa lenye kukidhi mahitaji ya hospitali ya Mji Kondoa?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Sannda anaita ‘kagari’ lakini gari zile zimetengenezwa kwa ajili ya mazingira ya Kiafrika na ukitazama jiografia ya Kondoa ukilinganisha na maeneo mengine ambayo gari zile zimepelekwa, nimtoe wasiwasi, wanasema ‘ukubwa wa pua siyo wingi wa makamasi’. Ile gari itamudu kufanya kazi iliyokusudiwa na katika maeneo ambayo gari kama zile zimepelekwa hatujapata malalamiko yoyote. Ni vizuri, wanasema ‘asiyeshukuru kwa kidogo hata ukimpa kikubwa hawezi kushukuru’. Ni jitihada za Mheshimiwa Rais na tuna kila sababu ya kuziunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, anauliza ni lini sasa itapatikana gari nyingine. Naomba nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inapunguza adha ya usafiri hasa kwa wagonjwa wetu, pale ambapo uwezo utaruhusu zikapatikana gari zingine tutaanza kuzipeleka maeneo ambayo hawakupata magari kabisa. (Makofi)
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, Kituo cha Afya cha Mbori kinachojengwa kinakaribia kukamilika pamoja na kwamba hakijapata milioni 500, lakini kwa kuwa kituo hiki kitahudumia Kata ya Lupeta, Kimagai, Godegode, Mlembule na Matomondo. Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kuwapeleka gari la wagonjwa kwa sababu litahudumia watu zaidi ya laki moja.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Lubeleje jinsi ambavyo amekuwa akiwapigania wananchi wake na hasa kuhusiana na suala zima la afya. Baada ya kupongeza ni vizuri Mheshimiwa Lubeleje kwa kushirikiana na wananchi na Halmashauri yake wakahakikisha hicho kituo cha afya ambacho anakisema hakijamalizika jitihada ziongezwe ili kiweze kukamilika kwa wakati. Pia nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali pale ambapo uwezo unaruhusu kupeleka gari za ambulance maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri. Hospitali yetu ya Mkoa wa Lindi ya Sokoine haina gari la Mganga Mkuu wa Mkoa na hii hupelekea Mganga Mkuu wa Mkoa kutumia gari yake ya binafsi (private car). Je, ni lini hospitali yetu ya Lindi ya Mkoa itapelekewa gari kwa ajili ya Mganga Mkuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Salma Kikwete kwa jinsi ambavyo amekuwa akilifuatilia jambo hili. Mimi binafsi ameshanifuata na suala hili nikalichukua na kulipeleka Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tulikuwa tunafanya logistics juu ya tatizo hili na ukubwa wake. Naomba nimhakikishie, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imelipokea kwa sababu siyo hali ya kawaida kwa Mganga Mkuu wa Mkoa kutumia gari yake binafsi katika kufanya shughuli za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba atupe muda kwa kadri tutakavyoweza tukipata nafasi ya kwanza kabisa suala hili tutalitatua.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, magari ambayo ameyazungumzia Mheshimiwa Sannda kwetu Mchinga tunayahitaji sana. Kituo cha Afya Kitomanga kinahitaji gari la wagonjwa lakini hakuna, nataka kujua tu, ni sifa gani ambazo haya magari yanapatikana ili tufuate hizo procedure kwa sababu taarifa tulizonazo humu ndani kuna Wabunge wamepewa mpaka magari mawili, wengine matatu, wakati wengine hatuna hata moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni hilo kwamba tutumie vigezo gani tupate haya magari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kuna sifa specific ambayo inabidi itumike ili kupata gari, hilo sina. Kinachozingatiwa ni uhitaji mkubwa wa maeneo ambayo yanahitaji magari na kwa uwiano kwamba zimepatikana gari ngapi ndipo zinagawiwa. Kwa hiyo, hakuna specific procedure kwamba sasa Mheshimiwa Bobali sasa hiyo sifa uwe nayo ili uweze kupata gari hiyo. Pale ambapo kuna uhitaji mkubwa na kwa kuzingatia jiografia ya maeneo husika na umbali wa wananchi kuweza kwenda kupata huduma hizo ndiyo sifa ambazo zinatakiwa.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Tatizo lililopo Kondoa Mjini halina tofauti na tatizo lililopo Jimbo la Singida Mjini. Kwa kuwa, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ndiyo kimbilio la wananchi wengi katika kupata huduma za afya, lakini hospitali hiyo haina kabisa gari la kubebea wagonjwa. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka gari la kubebea wagonjwa ili kuokoa vifo vya akinamama na watoto? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, jiografia na maeneo yanatofautiana. Kama hitaji kubwa kwa hospitali ya mkoa ni gari la wagonjwa na kwa sasa halipo, naomba nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Singida ahakikishe miongoni mwa gari zilizopo anateua gari moja itumike kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wakati Serikali ikijipanga kuja kupeleka gari la wagonjwa. (Makofi)
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nami niulize swali moja dogo la nyongeza. Hospitali ya Wilaya ya Manyoni pamoja na kuhudumia Wilaya ya Manyoni lakini inahudumia Wilaya ya Ikungi, Sikonge, Wilaya ya Bahi, Wilaya ya Chemba imezidiwa sana na haina kabisa gari la wagonjwa. Je, ni lini sasa Serikali itaipatia hospitali hii ya Wilaya gari la wagonjwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakubaliana Wabunge wote kwamba, nia ya Serikali na jinsi ambavyo inatenda katika kupunguza adha ya wagonjwa kwa maana ya uwepo wa magari sote ni mashuhuda tumeliona. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pale ambapo nafasi ya kifedha itaruhusu tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba maeneo yale yote ambayo yanahitaji kupelekewa gari za wagonjwa tunapeleka na kwa kufuata vigezo kama ambavyo nilivyotangulia kujibu katika swali langu la msingi.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini napenda kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki kimekuwa ni chanzo kizuri cha mapato katika maeneo ya majiji, manispaa na maeneo mbalimbali nchini. Hata hivyo, kumekuwa na kero kubwa sana kwa sababu ya kutosimamiwa vizuri kwa sheria hii. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri amewatangazia Wakurugenzi wa Halmashauri pia wangepelekewa maagizo haya kwa maandishi ili sheria hii iweze kusimamiwa na kupunguza kero ambayo ipo sasa hivi. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba nijibu na nipokee ushauri wa kutoka kwa Mheshimiwa Hamida na nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maelezo yake anasema kwamba chanzo hiki pamoja na kwamba ni cha uhakika lakini kimekuwa kero na mimi naomba niungane naye. Katika maeneo mengi unakuta kwamba mtumiaji anapo-park inakuwa kama ni suala la kuviziana, kwamba je, huyu atakosea ili adhabu iweze kutolewa. Naomba niwaagize Wakurugenzi wote kusimamia sheria hii lakini pia alama za parking ziwe ni zile ambazo zinaonekana kwa kila mtu ambaye anatumia gari ili anapo-park isije ikaonekana kwamba ni wrong parking.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na majibu mazuri ya Serikali, naomba nimuulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, tatizo la zahanati katika nchi yetu limekuwa likipungua siku hadi siku lakini kwa baadhi ya maeneo, maeneo mengi wananchi wameweza kuweka nguvu kazi zao kuhakikisha kwamba zahanati zinapatikana ili kupunguza vifo vya akina mama na watoto. Je, lini Serikali itamaliza yale maboma yote kuhakikisha kwamba tatizo hili linaisha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, swali hili linarandana sana na kituo cha afya kilichopo kule Lindi katika Kata ya Mnazi Mmoja. Je, ni lini watawahakikishia wananchi wa Lindi wanamaliza lile jengo pamoja na kwamba wameshawapa kiasi fulani cha fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la kumalizia maboma ambayo wananchi wameingiza nguvu zao, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Salma, naye ni shuhuda, jinsi ambavyo Serikali inaelekeza nguvu zake kuhakikisha kwamba maboma yote tunayamalizia hatua kwa hatua. Ndiyo maana tumeanza na ujenzi na ukamilishaji wa vituo vya afya 208 na juzi vimeongezeka viwili, tumekuwa na 210. Naomba nimhakikishie kwamba jitihada ambazo zimefanywa na wananchi Serikali itahakikisha kwamba tunamalizia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linalohusiana na Kituo cha Afya cha Mnazi Mmoja, naomba nimpongeze Mheshimiwa Salma kwa jitihada zake za kuwapigania wananchi wa Mkoa wa Lindi. Nilipata fursa ya kwenda kutizama kazi ya ujenzi wa Kituo cha Afya Lindi, kazi niliyoiacha ilikuwa inaenda vizuri. Naamini katika muda ambao tumekubaliana kwamba vituo vya afya hivi vijengwe kwa kuzingatia miezi mitatu na wananchi wa Lindi kwa maana ya Kituo cha Afya Mnazi Mmoja kwa jitihada nilizoziona na nguvu kazi na ari yao ya kujitoa, naamini ndani ya muda huo kituo cha afya kitaweza kukamilika. (Makofi)
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Naishukuru pia Serikali kwa kututengea Sh.500,000,000 za kujenga kituo cha Afya cha Gwanumpu na nimetoka Jimboni kazi sasa imeanza, ahsanteni sana.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo sasa nina swali moja tu. Pamoja shukrani hizo, Mheshimiwa Waziri kwa kuwa anajua kabisa Ubunge wangu bado mbichi; sasa ananiahidi nini kwa awamu hii inayofuata; kwamba itaanza lini ili Kata za Kiziguzigu, Kasanda, Rugenge, Gwarama na Nyamtukuza nazo zipate fedha za kujenga vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kama ambavo tumeainisha kwenye ilani yetu ya CCM kwamba kila kata tutajenga kituo cha afya na kila Wilaya ambako hakuna Hospitali ya Wilaya tutaenda kujenga, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, miongoni mwa maeneo ambayo tutahakikisha yanajengwa vituo vya afya ni yale ambayo yana upungufu mkubwa ikiwa ni pamoja na Wilaya yake ya Kakonko.
Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie, hakika pale ambapo bajeti itaweza kupatikana ikaongezeka hatutawasahau Kakonko na hasa tukiwa tunajibu fadhira ambazo wananchi wa Kakonko na hasa Buyungu walitoa kwa Chama cha Mapinduzi.
MHE. GIBSON B. OLE MEISEYEKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nimekuwa nikisubiria majibu ya swali hili kwa miaka mitatu sasa, lakini majibu niliyopewa siyo ya barabara ambazo Mheshimiwa Rais aliziahidi. Rais alipokuwa anaomba kura mwaka 2005 alitoa ahadi ya kilomita 12 ya bararaba inayoanzia Ngaramtoni kupitia hospitali ya Selian mpaka kwa Luhiyo kilomita 12. Alipochaguliwa 2012 akatuongeza barabara nyingine inayokwenda Hospitali ya Oltrumeti. Barabara zote hizi hazina lami mpaka sasa. Je, ni lini sasa Serikali itapata fedha ili iweze kuteleza ahadi hiyo ya Rais kwa barabara hizo ambazo alituahidi hizi nyingine alizozisema Mheshimiwa Waziri hazihusiani na swali langu?

Mheshimiwa Spika, pia ametaja kwamba barabara ya Sarawani inatengenezwa, ni kweli, lakini imekuwa ikitengenezwa kilomita 0.8 kwa takriban mwaka mzima sasa haijakamilika. Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kuongoza na mimi kwenda Arumeru Magharibi tukaangalie maendeleo na ubora wa barabara hii ya Sarawani - Oldonyosapuk ambayo kwa zaidi ya mwaka mzima inatengenezwa na bado haijakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nilikuwa na wasiwasi kwamba Mheshimiwa Mbunge angesema barabara hizi hazijaja kwenye jimbo lake lakini na yeye tunakubaliana kwamba barabara hizi zimejengwa kwenye jimbo lake, kwa hiyo, naamini kuwa Mheshimiwa Mbunge ana kila sababu ya kuipongeza Serikali kwa kujenga barabara hizo ndani ya jimbo lake.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ambazo tumetoa ni ahadi thabiti na kwa kadri uhitaji wa wakati unavyoruhusu ndio tunaenda kwenye barabara hizo. Kwa hiyo naomba nimhakikishie kwamba ahadi za Rais wetu aliyetangulia ambaye sasa amepokea kijiti Rais tuliyenayo bado ni ahadi za CCM, tutazitekeleza kwa kadiri bajeti itakavyoruhusu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anaomba fursa nikatazame hiyo barabara ambayo imekuwa ikitengenezwa ya kilomita 0.8, nalo ni jambo la kushukuru kwa sababu angeniambia kuwa haijaanza kutengenezwa kabisa then hata kuongea kwake ingekuwa tofauti. Naomba nimhakikishie kwa kadiri ratiba itakavyokuwa inaruhusu mimi nipo tayari kuambatana naye.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, Wilaya ya Same, ni Wilaya ambayo takribani, eneo lake katika Mkoa wa Kilimanjaro ni 40% ya eneo zima la Mkoa wa Kilimanjaro. Lakini Wilaya ya Same mara kwa mara inatengewa pesa kidogo sana inapewa pesa zilizoko chini ya wilaya ambazo ni ndogo zaidi ya wilaya ile. Naomba Serikali ione kwamba haioni umuhimu wa kutenga pesa zinazolingana na ukubwa wa Wilaya ile ya Same ambayo ni takribani 40% ya eneo lote la Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili nakuja kwenye barabara hii ya Hedaru – Vunta – Myamba barabara hii ni korofi mno, sijawahi kuona barabara kama hii, Awamu ya Nne niliwanyenyekea hapa Bungeni kwamba barabara ya Mkomazi, Kisiwani Same, waiweke kwa vipande vipande, walifanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa barabara hii yenye kilomita 42.2 hii TARURA Same wamefanya tathmini ya kutengeneza barabara yote kwa ujumla, wakapata ni bilioni 1.8.Je, Serikali hamuoni kwamba kwa sababu wananchi hawa wanahangaika mno mkatengeneza vipande vipande ili mmalize tatizo lote, kuliko mnavyochukua vimilioni viwili vitatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu kwanza kabla ya kujibu maswali mawili ya nyongeza nimpongeze kipekee Mheshimiwa Kilango Malecela jinsi ambavyo amekuwa akipigania wananchi wake wa Same na sisi sote ni mashahidi Kiwanda kile cha Tangawizi kimejengwa ni kwa ajili ya kazi kubwa aliyofanya yeye.

Mheshimimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba mgawanyo wa fedha umekuwa hauendani na uhalisia na hili ni swali ambalo limekuwa likiulizwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI baada ya kuliona hilo sasa hivi tuna-commission consultant kwa ajili ya kuja na formula nzuri itakayosaidia ili tunapogawa fedha twende na uhalisia. Kwa sababu formula inayotumika ndiyo iliyokuwa inatumika mwanzo kabla TARURA haijaanza kufanya kazi. kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Kilango Malecela na Wabunge wengine tuvute subira kwa sababu tayari consultant anafanya kazi atatuletea majibu na formula ambayo itakuwa nzuri kwa kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lake la pili anaona iko haja kwa ajili ya ukorofi wa ile barabara tuanze kujenga kwa kiwango cha lami walau kilometa chache chache at the end tuje tukamilishe kilometa zote 42. Ni wazo jema kwa sababu vinginevyo tunakuwa tunarudia fedha inatumika lakini kwa mazingira na jiografia ya barabara ambayo Mheshimiwa ametaja iko haja kubwa sana.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, barabara za Mkoa wa Kilimanjaro zikiweko za Same pamoja na za Vunjo na mkoa wa ujumla ziko kwenye maeneo ya mwinuko. Na barabara zote hizi, zinavyotengenezwa zinawekewa fedha kidogo ambazo sasa haziendani na hali halisia ya soil property au tabia ya barabara hizo. Je Serikali haioni umuhimu, wa kutafuta aina ya material ambayo ni nzuri na ambayo siyo ghari kama ilivyo beachmen ili kuweza kufanya barabara hizo ziweze zikapitika kwa urahisi na kuongeza uchumi wa Mkoa wa Kilimanjaro na Tanzania kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo ambalo Mheshimiwa Mbunge anatoa ni wazo jema na sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI tumekuwa tukifanya majaribio na tumeanzia Wilaya ya Bihalamuro tulienda na Mheshimiwa Mukasa. Kuna stadi ambayo inafanyika namna ya kuweza kujenga barabara kwa gharama nafuu lakini barabara ambazo zitaweza kudumu kwa kipindi kirefu. Kwa hiyo, ni wazo ambalo tunalifanyia kazi hakika baada ya kujiridhisha juu ya uwezo wa barabara hizo kuhimili kudumu ni wazo ambalo tutalifanyia kazi kujenga barabara zetu kwa gharama nafuu lakini ambazo zitadumu kwa muda mrefu.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante, Wilaya ya Ludewa eneo la Kandokando mwa Ziwa Nyasa kuna vijiji takribani kumi na mbili, gari, baiskeli wala pikipiki haijawahi kufika huko. Niishukuru Serikali kuna kipande cha Mwambahesa kwenda Makonde, kimeanza kufanyiwa kazi. Je, TARURA inafikiriaje sasa kutuongezea wananchi wa Ludewa hususani waishio kandokando wa Mwambao wa Ziwa Nyasa kutoka eneo la Makonde mpaka kihondo ili tuweze kupata barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kutembelea jimbo la Mheshimiwa Ngalawa, kama kuna maeneo ambayo kuna changamoto ya milima maana kule milima ya Livingstone ndio inapita kule, ukanda ule, ni ukanda wa kutizama kwa jicho tofauti kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Mheshimiwa Mbunge naye amekiri kwamba kuna kazi nzuri ambayo inafanyika juu ya kuhakikisha kwamba wananchi wale wanakuwa na barabara ambayo inapitika vipindi vyote. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba kila eneo ambalo wako wananchi wetu, barabara zinapitika vipindi vyote, kwa kadiri bajeti itakavyoruhusu na yeye pia tutahakikisha kwamba wananchi wake wanapata barabara ya uhakika.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza, kwanza naipongeza Serikali kwa kutupatia pesa katika kituo cha Afya cha Sakala milioni mia nne na Usunani milioni mia nne katika Wilaya ya Ngorongoro Mkoa wa Arusha. Nilitaka kufahamu katika kwa kuwa vituo hivi vinakamilika siku si nyingi je Serikali imejipangaje, kuhakikisha inatuletea vifaa tiba na raslimali watu katika vituo hivi viwili vya Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Catherine jinsi ambavyo amekuwa akiwapigania wananchi wa Mkoa wa Arusha hususani kuhusiana na suala zima la Afya, baada ya pongezi hizo naomba nimjibu Mbunge na kwa Wabunge wote ambao wana maswali kama hayo kuhusiana na lini vifaa na wataalam watapelekwa ili hayo majengo ambayo yamekamilika yaanze kufanya kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ambayo tunaikaribia 2019/2020 sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI, fedha nyingi tumetenga ili tuweze kuhakikisha kwamba tunapata vifaa vyote ili Vituo vya Afya vianze kufanya kazi iliyokusudiwa. Kwa sababu utakubaliana na mimi kwamba ukiwa na majengo mazuri bila kuwa na vitendea kazi itabaki kuwa White elephant na sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI hatutaki kuwa sehemu ya mzigo huo. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge mchakato uko katika hali nzuri ili tuhakikishe kwamba Vifaa vinapatikana na Watumishi wa kutosha wanapatikana ili majengo yakishakamilika huduma ianze kutolewa.
MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwenye jimbo la Chalinze hakuna Hospitali ya Wilaya, mwenzi mmoja uliopita tulimsumbua Mheshimiwa Kangi Lugola tulikutana tumepata ajali, magari yetu yakaanza kusoma majeruhi, tukauliza shida ni nini? TAMISEMI kwa nini? Mnaweka hela Kibaha Mjini Kibaha Vijijini na kuna Tumbi? Kwa nini hamuwezi kupeleka hela katika Jimbo la Chalinze kupata Hospitali ya Wilaya kwa sababu kuna umbali mrefu watu wakipata ajali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, najua iko kiu kubwa sana Waheshimiwa Wabunge maeneo mengi ambayo wangependa Hospitali za Wilaya na tunaita Hospitali za Halmashauri ziweze kujengwa. Sasa katika hii ambayo umesemea kuhusiana na Chalinze kuwa na Hospitali ya Wilaya, sina uhakika katika orodha ya Hospitali za Halmashauri ambazo zimetengewa bilioni 1.9 kama Chalinze ipo au haipo. Kama inakidhi vigezo katika bajeti tunayoenda nayo kuna Hospitali tisa nazo tutaziingiza nje ya zile 67 sasa, kama na Chalinze ni mojawapo hilo sioni kama…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mkuranga mpaka leo kwa muda mrefu haina x-ray.Ni lini sasa Serikali itahakikisha hospitali ile inakuwa na x-ray kusudi kuwasaidia wananchi wa pale Mkuranga?Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ruth Mollel kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya nyongeza katika maswali ya nyongeza kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha maeneo yote ambayo majengo yapo, vifaa vinakuwepo na wataalam wa kutosha wanakuwepo. Kwa hiyo, ni vizuri tukajua hii Hospitali ya Mkuranga ambayo naamini ni miongoni mwa hospitali ambazo zinatakiwa ziwe na huduma hiyo, nini kilikosekana ili katika vifaa vitakavyopelekwa na yenyewe ipate hiyo X-ray.
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika,ahsante kwa kunipa muda niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza niipongeze sana Serikali na majibu imejibu vizuri, imepeleka faraja kwa wananchi wa Jimbo la Manyoni hasa Manyoni Mashariki, niombe kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara hii tunayoizungumzia ya Chikuyu Majiri-Ikasi, kipande kile cha mwisho kabisa cha kilometa 40kwa maana ya Majiri kwenda Ikasi, ni miaka zaidi ya 40 hakijapata fedha ya matengenezo ya mara kwa mara.

Naomba tu kuhakikishiwa na kuwahakikishia wananchi wangu wa Manyoni ni lini au ni bajeti ya mwaka huu watatoa fedha ya kutengeneza barabara hii maana ni miaka zaidi ya 40? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtuka Motokari kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la nyongeza anasema miaka zaidi ya 40 barabara hii haijatengewa fedha yoyote, wakati mwingine mipango ya Mwenyezi Mungu inakuwepo ili mtu fulani aweke alama, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mtuka laiti barabara hiyo ingekuwa imetengenezwa isingekuwa kwake yeye rahisi kuacha alama, naomba nimhakikishie ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa na hasa baada ya kujua gharama ya daraja ambalo ndiyo kubwa zaidi na yeye atakuwa ameacha alama muhimu sana kwa wananchi ambao miaka zaidi ya 40 ilikuwa haipitiki.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika,nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya kutoka Singida – Kinyeto - Mahojoa - Sagara yenye urefu wa kilomita 42 ambao tuliiombea kwa Mheshimiwa Rais kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kweli kwa sasa imeharibika kwa kiwango kikubwa sana. Je, Serikali ipo tayari sasa kutenga fedha za ziada za dharura katika kuhakikisha kwamba madaraja yaliyovunjika katika msimu huuna barabara yanarekebishwa?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Monko anakiri kwamba barabara hiyo ilikuwa imejengwa kwa kiwango cha lami na mvua imenyesha madaraja yameanza kubomoka. Tukubaliane kwamba kila neema wakati mwingine inakuja na adha yake, kama ambavyo ilikuwa nia ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika, ni vizuri tukaenda tukajua uharibifu uliotokea na gharama zinazohitajika ili kuirudisha barabara katika hali yake ya kuweza kupitika kama tunavyotarajia kwa wananchi wetu.
MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa msaada huo katika sehemu hizo mbili zilizotajwa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini Serikali itazisaidia Vituo vya Afya vya Mtamba pamoja na Kisaki ambavyo mchakato wake Serikali ulishaanza kushughulikia?

Je, ni lini Serikali itapeleka au itasaidia Hospitali Kuu ya Mkoa wa Morogoro mashine ya CT-Scan ili kuokoa maisha ya watu ambao yanapotea bure kwa ajili ya kukosa huduma ya mashine hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetaja katika jibu la msingi Wilaya ya Morogoro Vijijini ambayo Mheshimiwa anatoka ni miongoni mwa Wilaya ambazo zimepata nafasi ya kujengewa Hospitali za Wilaya na tumeanza kupeleka shilingi bilioni 1.5 lakini ili ikamilike tunahitaji tunahitaji jumla ya shilingi bnilioni 7.5. Lakini mwenyewe anakiri kwamba tayari tumeanza kujenga Kituo cha Afya pale Duthumi, najua kabisa kiu ya Mheshimiwa Mbunge kwamba na maeneo mengine Vituo vya Afya vijengwe naomba nimuakikishie kwamba ni azima ya Serikali kwa kadri bajeti inavyoruhusu tumeanza na vituo 350 lakini azma kuhakikisha kwamba katika kata zetu zote kwa kadri bajeti itakavyo kuwa inaruhusu kama ambavyo tumeahidi kwenye ilani ya CCM tunaenda kutekeleza.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mwongozo wetu wa Wizara ya Afya huduma za CT-Scan zinapatikana kuanzia Hospitali za ngazi ya Rufaa za Kanda. Lakini baada ya kuwa tunafanya mapitio katika hii sera mpya tunajaribu kuangalia huduma sasa hivi katika nchi yetu zimekuwa sana na tumeona kwamba baadhi ya hospitali za mikoa ambazo ziko kimkakati. Lakini vilevile huduma hizi za CT-Scan zinahitaji utaalamu wa hali ya juu kuweza kuzitumia ambazo zingine huduma hizi hazipatikani katika Hospitali za Mikoa, Hospitali Wilaya na kushuka chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mkakati wetu sisi kama Serikali nikujaribu ku-identity mikoa ile ambayo ni ya kimkakati ikiwa ni pamoja na Morogoro kwa sababu kuna aya inapita pale ili huduma hizi ziweze kupatikana kwa lengo kuhakikisha kwamba tunazuia ajali baadhi ya Mikoa lakini hatutaweza kuzishusha huduma chini ya ngazi ya hospitali ya rufaa Mikoa kwa sasa.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Wizara wanakiri kwamba kumekuwa na changamoto kutokana na maboma mengi ambavyo yamekuwa katika Halmashauri zetu, lakini pamoja na mkakati wao, walipofanya utafiti waligundua kwamba Halmashauri hazina uwezo wa kukamilisha maboma yote yanayojengwa kule kwenye Majimbo yetu; na ni ukweli usiopingika kwamba Mfuko wa Pamoja bado hauwezi kutosheleza:-

Sasa ni nini mkakati thabiti hasa wa Serikali kuhakikisha aidha kuwe na mkakati wa kusema kiasi cha maboma kinachopaswa kujengwa kwenye kila Halmashauri ili wao waweze kumalizia au tuendelee na kusubiri ujenzi wa Vituo vya Afya na Zahanati kutoka Mfuko wa Pamoja?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu kwenye majibu yangu ya msingi; na Mheshimiwa Mbunge naye atakubaliana name kuhusu azma njema ya Serikali ambayo anaiona jinsi ambavyo tunapambana kuhakikisha kwamba tunapeleka huduma kwa maana ya kujenga Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na Zahanati. Ndiyo maana katika majibu yangu ya msingi nimejibu kwamba ni vizuri tukafungua avenue pale ambapo Halmashauri zile ambazo ambazo zina uwezo, lakini pia kwa kushirikisha wananchi na wadau wengine tuendelee kujenga kwa kushirikiana na Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunasogeza huduma za matibabu karibu kabisa na wananchi, lakini pia vipaumbele ni vingi. Kwa hiyo, ni vizuri tukashirikiana pale bajeti inaporuhusu, Serikali inapeleka lakini pia na Halmashauri na wadau wengine ni vizuri wakashiriki katika suala hili muhimu sana kwa wananchi wetu.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa, naipongeza Serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya, vilevile upanuzi wa vituo vya afya, tunapongeza sana jitihada hizo za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na majibu hayo ninayo maswali mawili ya nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ni kweli imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ilemba lakini katika bajeti zake mfululizo imekuwa ikitenga fedha kwa maana ya kumalizia jengo hilo lakini mfululizo wa miaka karibu minne Serikali haijatoa fedha. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba eneo hilo lina mwingiliano mkubwa sana wa watu kutokana na biashara ya mpunga na samaki na kunakuwa na milipuko mingi ya magonjwa, wananchi wanakufa, wanapata taabu sana. Naomba Serikali sasa itambue kilio hicho iweze kutupatia fedha kumalizia kituo hicho cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ujenzi wa Kituo cha Afya Ilemba, vipo vituo vingine vilishaanza kujengwa katika maeneo ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, Vituo vya Afya vya Muze, Kaoze, Kiteta, Kalambanzite pia zahanati 12 na hii yote inatokana na sera ya kila kata kuwa na kituo cha afya na kila kijiji kuwa na zahanati, jambo ambalo Serikali yenyewe imepanga na tumewahamasisha wananchi. Ni nini kauli ya Serikali katika kukamilisha majengo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu, naomba uniruhusu kipekee nimpongeze Mheshimiwa Malocha na wananchi wake wa Jimbo la Kwela kwa jinsi ambavyo wameitikia wito mkubwa wa kuhakikisha kwamba ujenzi unafanyika. Kipekee, naomba nimpongeze hata Mkuu wa Mkoa, nilimuona akishiriki yeye mwenyewe katika kuchimba msingi katika ujenzi wa hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, naomba niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, kwanza tunathamini sana jitihada ambazo zinafanywa na yeye binafsi na wananchi wake. Kwa kadri bajeti ya Serikali
inavyoruhusu, maeneo yote ambayo ameyataja, pia hajataja Kituo cha Afya Mpui, naomba nimhakikishie, kwa kadri bajeti itakavyoruhusu hatuwezi tukaacha nguvu za wananchi zikapotea bure. Iko kwenye Ilani yetu ya CCM, tumeahidi, tutatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe tuliomba fedha kwa ajili ya vituo vya afya hasa ikizingatiwa kwamba hatujapata hata kituo kimoja mpaka leo na tuliomba kwa ajili ya Kituo cha Afya Kichiwa ili kiweze kutoa huduma ya upasuaji lakini pia Kituo cha Afya cha Lupembe ambapo tumejenga huduma ya upasuaji kupitia mapato ya halmashauri na tumejenga jengo dogo la akina mama kupitia mchango wa Mbunge na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanataka kujua ni lini Serikali italeta hizo fedha kama zilivyopelekwa kwenye halmashauri nyingine na sisi Jimbo la Lupembe tuweze kupata angalau zile shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuwa na vituo angalau viwili vitakavyotoka huduma ya upasuaji? Sasa hivi akina mama wanapata shida sana na wanatembea umbali mrefu kwa ajili ya kutafuta huduma hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, katika maeneo ambayo hatukujenga kituo cha afya ni pamoja na Jimboni kwake Mheshimiwa kule Lupembe. Mheshimiwa hajataja kuwa miongoni mwa wilaya ambazo zinakwenda kujengewa hospitali za wilaya ni pamoja na wilayani kwake. Pia amewahi kupata fursa ya kuongea na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana akamuahidi kwamba ikipatikana fursa ya kupata vituo hata viwili au kimoja, hatutasahau kituo chake. Naomba wananchi waendelee kuunga mkono Serikali, tumeahidi, tutatekeleza.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti,ahsante; nitakuwa nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto kubwa kwenye vituo vyetu vya afya na zahanati na changamoto kubwa ni upatikanaji wa magari ambayo yanawasafirisha wagonjwa (ambulance). Ningependa kufahamu katika vituo hivi ambavyo tunavyo katika Jimbo la Kalenga vituo kama vinne, tuna gari mbili tu lakini moja linatumika kupeleka wagonjwa katika Jimbo zima. Ningependa kufahamu, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba tunaongezewa gari hasa katika Kituo cha Afya cha Mgama? (Makofi)
Tuna changamoto kubwa ya madawa kwenye vituo vyetu vya afya na zahanati mbalimbali hasa katika Jimbo langu la Kalenga. Ningependa kufahamu kwa sababu vituo hivi vya afya vinatumika kwa wananchi wengi. Ningependa kufahamu katika Kituo cha Ng’enza, Kituo cha Itwaga na Kituo cha Muwimbi ni lini sasa madawa yataanza kupelekwa kwa sababu kuna vituo vimeshafunguliwa kupitia mwenge lakini mpaka sasa hivi havina madawa na havijaanza kufanya kazi, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIKOA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake mawili ya nyongeza la kwanza anaulizia juu ya suala zima la upatikanaji wa gari (ambulance). Naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mgimwa, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba gari zinapatikana kwa kadri hali inavyoruhusu na hivi karibuni tunatarajia kupata gari 70 na katika gari hizo 70 ambazo tunatarajia kuzipata ni matarajio ya Serikali kwamba tutalenga katika maeneo ambayo yana upungufu mkubwa sana. Nina amini eneo la kwake kama ni miongoni mwa maeneo ambayo yana upungufu mkubwa litakuwa considered.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaulizia juu ya vituo vya afya vitatu ambavyo amevitaja kwamba vituo vya afya hivyo dawa hazipatikani. Naomba nikiri kwa fursa niliyopata ya kuzunguka katika maeneo yote ya Tanzania kwa mara ya kwanza ndiyo nasikia kwamba kuna vituo vya afya ambavyo havipati dawa. Ni vizuri tuwasiliane na Mheshimiwa Mbunge ili tujue tatizo ni nini kwa sababu ni azma ya Serikali kuhakikisha vituo vyote vinapokamilika na dawa ziweze kupatikana ili huduma iliyokusudiwa na Serikali iweze kupatikana kwa wananchi.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kututengea hizi pesa kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya, lakini kipekee nachukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Jafo kwa jinsi ambavyo nimekuwa nikimsumbua kuhusiana na Vituo vya Afya na Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo, kulingana na jiografia ya Wilaya yangu, ninaomba kuuliza swali. Kwa kuwa tuna vituo vitatu kwenye Tarafa nne na kwenye Kata 24: Serikali iko tayari kututengea kituo kingine kimoja? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kyerwa tuna upungufu mkubwa wa watumishi. Kwenye kituo kingine unakuta kuna watumishi wawili kwenye Zahanati moja: Je, Serikali iko tayari kututengea watumishi wa kutosha ili wananchi waweze kupata huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kwa niaba ya Serikali nipokee pongezi kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge. Katika hali ya kawaida, mtu anayeshukuru tafsiri yake ni kwamba anaomba kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga Vituo vya Afya kwa kadiri nafasi ya kibajeti itakavyoruhusu. Jiografia ya Kyerwa hakika ni jiografia ambayo ina utata mkubwa, Jimbo ni kubwa. Naomba aendelee kuiamini Serikali, kwa kadiri bajeti itakavyoruhusu na tutakavyokuwa tunaendelea kujenga Vituo vya Afya, naye tutamkumbuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna swali lake la pili; anaomba kuongeza idadi ya watumishi ili waweze kutoa huduma ambayo inastahili kwa wananchi wake. Sasa hivi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeomba kibali cha kuweza kupata nafasi za kuajiri. Kwa kadiri nafasi zitakavyokuwa zimepatikana, hakika katika usambazaji tutahakikisha maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa yanazingatiwa. Naamini na eneo lake ni miongoni mwa maeneo hayo. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika,
kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, ninaomba kutoa maelezo ya nyongeza kuhusu uhaba wa watumishi, hasa afya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Serikali inafanya jitihada za kujenga Vituo vya Afya na Zahanati nchi nzima. Tunakiri kwamba watumishi hawatoshi, ndiyo maana kwa kushirikiana na TAMISEMI tunafanya utaratibu wa kuongeza. Nimesimama hapa kueleza kwamba, sisi upande wa Wizara ya Utumishi na Utawala Bora tutaweka kwanza kipaumbele katika Zahanati na Vituo vya Afya vipya ambavyo havijaanza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Viongozi wa Mikoa, Waheshimiwa Wabunge mkiwasimamia, kuhakikisha wanapoleta maombi watuletee kwamba Zahanati mpya inahitaji watumishi kadhaa, Kituo cha Afya kipya kinahitaji watumishi kadhaa. Pamoja na uhaba uliopo, lengo ni kwamba Vituo vyote vya Afya na Zahanati zote mpya zifunguliwe mara moja, ndiyo tutawapa kipaumbele, kwa sababu sehemu nyingine huduma bado zitaendelea kutolewa japo kwa upungufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda kwa ruhusa yako pia, nijibu suala la uhaba wa Walimu. Sasa hivi baada ya kufungua mwaka mpya huu wa masomo, Walimu wengi wamestaafu mwaka 2018, wengine wamefariki. Sisi upande wa Utumishi tutaanza kwanza kujaza idadi ya Walimu waliostaafu mwaka 2018, ili tuwe na kiwango cha Walimu kama waliokuwepo mwaka 2018, baada ya hapo tutaendelea na zoezi la kuajiri Walimu wapya.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona na kunipa nafasi, lakini pia naomba nimshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu hayo, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; Mheshimiwa Waziri Mkuu pia alifanya ziara katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala na kwa kuona hali ilivyokuwa na hasa wananchi walivyojitolea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano katika kukabiliana tatizo la afya, alikubali pia kutushika mkono kwa kutupatia shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Isaka. Nataka kufahamu ni hatua gani imefikiwa katika utekelezaji wa ahadi hiyo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu?

Swali la pili; kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kuna Halmashauri 67 ambazo zimepatiwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi kwa Hospitali za Wilaya, kwa bahati mbaya Halmashauri ya Wilaya ya Msalala haina hospitali ya Wilaya na haiko katika hizi Halmashauri 67. Nataka kufahamu: Je, itawezekana sasa kwa awamu hii ambayo itakuwa ni ya pili mwaka 2019/2020 Halmashauri hii nayo ikatengewa hiyo fedha ili na yenyewe iweze kupata Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kipekee kwanza naomba nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Maige na wananchi wake jinsi ambavyo wamekuwa wakijitolea katika suala zima la afya, wamejenga maboma mengi kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu ametembelea Msalala na akahaidi kwamba na Kituo cha Afya Isaka nacho kingeweza kupatiwa fedha; ni ukweli usiopingika kwamba Isaka ni miongoni mwa eneo ambalo lina watu wengi na iko haja ya kuhakikisha kwamba kunakuwa na Kituo cha Afya ili kupunguza adha ya wananchi wengi kupata huduma ya afya. Naomba aendelee kuiamini Serikali kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi kwamba kwa kadri fursa ya fedha inapopatikana ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba ahadi zote za viongozi wa Kitaifa tunazitekeleza. Nasi bado tunakumbuka hiyo ahadi, naomba Mheshimiwa Maige avute subira.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni kwamba katika Halmashauri 67, Halmashauri yake haikuwa miongoni mwa zile ambazo zilipata fursa ya kujengewa hospitali. Sina uhakika katika orodha ya hivi sasa hivi tuna jumla ya Halmashauri 27 ambazo katika bajeti, tutakapokuja kuomba fedha tutaenda kuongeza fedha katika Halmashauri nyingine 27. Tuombe Mungu katika hizo 27 na yake iwe miongoni mwake.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yake kwa swali la msingi la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, nataka niwahakikishie tu kwamba bado kuna ongezeko kubwa la watoto hawa katika Barabara ya Sita, Barabara ya Tisa hapa Dodoma na katika Soko la Dodoma la Matunda na Mboga Mboga.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie kwamba hali hii Jiji la Dodoma wanaifahamu. Sasa utuambia mwarobaini au mkakati madhubuti ama mkakati mahususi wa kuweza kuwasaidia watoto hawa, kwa sababu kila siku ongezeko hili kidogo linatisha.

Mheshimiwa Spika, swali la pili Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba baadhi ya watoto hawa wazazi wao tayari wamefariki kwa maradhi mbalimbali, lakini kuna baadhi ya watoto hawa wazazi wao wako hai na wako katika maeneo ya karibu katika maeneo mbalimbali. Sasa wanasema kwamba watatoa elimu, atuambie mkakati wa ziada kuhakikisha kwamba wale watoto ambao wazazi wao wapo hai wanachukua hatua gani ya dharura kuhakikisha wazazi hawa wanapatikana na suala hili kulikomesha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza suala kwamba kuna ongezeko, hiyo inakuwa kidogo ni relative term, kwa sababu ongezeko hilo unalipima kuanzia lini? Kama nilivyojibu katika swali langu la msingi, kwa mujibu wa sheria ni wajibu kuhakikisha kwamba mtoto analelewa katika mazingira mazuri. Jitihada zimefanywa na Serikali kwanza kuwatambua hawa watoto.

Kwa mfano, kwa Mkoa wa Dodoma na hasa Jiji la Dodoma, jitihada za makusudi zimefanyika kwanza kuhakikisha kwamba wale watoto ambao wana wazazi wao wanarudishwa na kuunganishwa na familia kwa sababu wajibu wa kwanza wa kumlea mtoto ni wa familia.

Mheshimiwa Spika, kuna cases kama ambazo watoto wanalazimika kuondoka katika mazingira na kwenda katika mazingira hayo kwa sababu aidha, wameondokewa na wazazi wao kwa magonjwa masuala kama hayo, ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimesisitiza kwamba ni wajibu wetu sisi kama jamii kwa ujumla kuhakikisha kwamba watoto ambao wanatakiwa kwenda shule waende shule na kuna mpango wengine wanaweza kupelekwa VETA. Ni jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba watoto hawaishi katika mazingira magumu.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; barabara hii ninayoiombea ni ya kutoka Makao Makuu ya Wilaya kwenda mkoani, Wilaya ya Songwe ni mpya kabisa, kwa hiyo hatuna barabara inayounganisha wilaya na mkoa, kwa hiyo ningependa Serikali ifanye uharaka zaidi kwa sababu wale wananchi wanapitia Mbalizi ambako ni mbali sana. Kama itakuwa inatenga milioni 63 kila mwaka maana yake itachukua miaka sita kuja kupata hii barabara, nataka Serikali angalau iniongezee fedha kutoka milioni 63 mpaka milioni 300 ili tuweze kumaliza hii barabara kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Rais alipokuja Wilaya ya Songwe tulimwomba kilometa nne kwa ajili ya kufanya Mji wa Mkwajuni, Makao Makuu ya Wilaya yawe salama na yawe safi. Sasa ni lini Serikali itatupa fedha kwa ajili ya kilometa nne za lami pale Mji wa Mkwajuni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mulugo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu kwenye majibu yangu ya msingi, yeye mwenyewe anakiri kwamba ameona nia ya Serikali ya kuhakikisha kwamba kwanza tunatambua kwamba tunataka tutumie kilometa ili wananchi wasiendelee kuzunguka na tumeanza kujenga hayo madaraja. Katika majibu yangu ya msingi nimemhakikishia kwamba ni vizuri tukawa na tathmini kujua gharama halisi ili hata hicho kiasi cha fedha kinavyotafutwa tuwe tunajua tunatafuta kwa ajili ya kazi gani ambayo inatakiwa ifanyike. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali tunatambua iko haja ya kuhakikisha kwamba wanafika Makao Makuu ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, anasema iko ahadi ya kilometa kwa ajili ya lami ili na wao katika makao makuu ya wilaya wafanane na makao makuu ya wilaya zingine. Naomba nimhakikishie Mhesimiwa Mbunge; ahadi zote za Viongozi wa Kitaifa tunazitekeleza na kwa Mkoa wa Songwe tumeanzia Makao Makuu kwa maana ya Momba, tunaanza kuweka kilometa moja, lakini pia na Mbozi. Naomba hatua kwa hatua, hakika ahadi zote za Viongozi wa Kitaifa sisi tutakwenda kuzitekeleza.
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu hayo ya Serikali, kwenye Kituo cha Afya cha Ulaya nilishauliza hapa mara nyingi kwamba Serikali itatusaidiaje maana ni kituo cha muda mrefu na kimeshachakaa na Serikali iliahidi kwamba itatupatia fedha za kuweza kukarabati kituo hichi cha Ulaya. Je, ni lini sasa Serikali italeta pesa kwenye kituo hiki cha Ulaya ambacho kimechakaa sana na ni kituo muhimu kinachituhudumia Kata za Ulaya, Muhenda, Zombo pamoja na Masanze?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Kituo cha Afya cha Malolo kinajengwa kwa nguvu za wananchi wakishirikiana na Mbunge na Halmashauri na sasa kimefikia kwenye kiwango cha lenta. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza nguvu za wananchi ambazo sasa hivi zimeonekana ili waweze kujipatia huduma katika Kituo cha Afya cha Malolo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Haule Joseph, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo katika swali lake la nyongeza anaongelea Kituo cha Afya cha Ulaya ambacho kimechakaa, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine wote, ni ukweli usiopingika kwamba vituo vya afya ambavyo vimepatiwa fedha kwa ajili ya ukarabati na ujenzi vinaonekana viko bora kuliko vile ambavyo vilikuwa vya siku nyingi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vile vituo vya afya ambavyo vilijengwa miaka hiyo na hadhi yake haiendani na vituo vya afya vya sasa, iko katika utaratibu wa kuhakikisha kwamba vinakarabatiwa ili vilingane na hadhi ya sasa. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali kama ambavyo tumeweza kupeleka fedha katika hivyo vituo vya afya na zahanati yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anaongelea jitihada ambazo zinafanywa na halmashauri pamoja na nguvu yake mwenyewe nampongeza kwa sababu suala la afya linahusu jamii yote ikiwa ni pamoja na Waheshimiwa Wabunge. Pale ambapo wananchi wamejitoa kwa ajili ya kujenga vituo vya afya Serikali na sisi tunaunga mkono kwa sababu ndio azma ya Serikali nayo iko kwenye ilani yetu ya CCM.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kata ya Mnyagala ni kata ambayo ina idadi ya watu wengi na vijiji kadhaa ambavyo hakuna huduma ya kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika eneo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Moshi Sulemani Kakoso, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi wana hamu vituo vya vingi vijengwe na nimepata fursa ya kwenda jimboni kwa Mheshimiwa Kakoso tukaenda mpaka Mwese kule kuna kazi nzuri sana inafanyika ya ujenzi wa kituo cha afya kama ambavyo kazi nzuri imefanyika Kituo cha Afya Mwese, naomba nimtoe wasiwasi kwamba hata hicho kituo ambacho ana-propose kwa kadri nafasi itakavyoruhusu hatua kwa hatua tutahakikisha tunawasogezea wananchi huduma ya kupata matibabu ya afya kwa jirani.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Ikungi Mashariki halina kabisa kituo cha afya. Je, ni lini sasa Serikali itajenga vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matembe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo anaongelea Ikungi Mashariki wakati mwingine ataongelea Ikungi Magharibi, lakini niombe tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo tumekuwa tukitekeleza na tumefikisha hivyo vituo vya afya 352, safari tunayo na tutazingatia maeneo yenye uhitaji mkubwa na sasa kama na eneo ambalo Mheshimiwa Mbunge analitaja kwamba lipo mbali na lina population kubwa, naomba nimhakikishie kwamba katika awamu inayokuja tutazingatia maombi yake.
MHE. SUSAN A. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Sekta ya afya kwa ujumla wake ina tatizo kubwa sana la watumishi, takribani asilimia 48 hakuna watumishi na hii imeathiri zaidi kwa sababu ya zoezi zima la uhakiki wa vyetii feki, ambapo tuliambiwa baadhi ya vituo ya afya vilifungwa. Nataka kujua nini mkakati wa Serikali
pamoja na kwamba wanajenga vituo, wana mkakati gani wa kuhakikisha kwamba vituo hivi vya afya vyote vinapata wataalam ili lipunguze tatizo kubwa la akinamama na watoto ambao wanafariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lyimo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba mahali popote ambapo vituo vya afya vinajengwa vinakamilika, zahanati zinajengwa zinakamilika, hayabaki yakawa majengo ambayo tunayatazama, tutahakikisha kwamba vifaa vinapelekwa na wataalam wanapelekwa. Mheshimiwa Lyimo ni shahidi, siku tukiwa ndani ya Bunge hili Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Mkuchika alisema kama yupo Mbunge yeyote ambaye eneo lake zahanati imefungwa au kituo cha afya hakina wataalam kabisa apeleke orodha, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma zinatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikuhakikishie, kuna kipindi ambacho tulitangaza nafasi especially kwa ajili ya Madaktari tuliweza kufanya mopping, hakuna Daktari hata mmoja ambaye alikuwa ame-qualify akabaki bila kuajiriwa. Ikafikia mahali ambapo Madaktari wote wameajiriwa na wengine hawajaripoti. Kwa hiyo pia tuna tatizo juu ya wataalam wenyewe kuwepo maana na demand nayo ni kubwa si kwa Tanzania peke yake, wengine wanaenda kutafuta green pastures outside this country.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu hayo kutoka Serikalini, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ilemela ilifanikisha kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya katika Kata ya Buswero na walifanikisha kukamilisha majengo ya OPD na vilevile jengo la magonjwa ya dharura. Hata hiyo, kutokana na changamoto zilizokuwa pale, wakaona hapafai kuwa na Hospitali ya Wilaya maeneo yale wakaanzisha ujenzi katika Kata ya Bugogwa:-

Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa majengo yale kuanza kutumika sasa kama Kituo cha Afya, kwa sababu yanakidhi haja hiyo ya kuwa kituo cha afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, swali langu la pili nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kutujengea Kituo cha Afya cha Malya Wilayani Kwimba. Kwa kweli ni kituo kizuri kinatoa huduma kwa wananchi wengi Wilayani humo, lakini kimekuwa na changamoto zifuatazo: hakina Mganga Mkuu na mhusika mkuu pale ni Clinical Officer; vile vile hakina mtaalam wa Maabara, hakina chumba cha upasuaji, hakina Daktari wa Akina Mama na Watoto; na bahati nzuri Naibu Waziri, Mheshimiwa Waitara ameshafika katika hiki kituo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, swali langu ni moja: Je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba changamoto hizi zinapungua ili tuweze kupunguza vifo vya akina mama na watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza Mheshimiwa Maria anauliza juu ya umuhimu wa eneo ambalo lilikuwa limeshaanza kujengwa Hospitali ya Wilaya lakini ikaonekana kwamba hapafai ni bora kikajengwa kituo cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze kwa dhati. Hata pia Mheshimiwa Angelina Mabula amekuwa akiliongelea suala hili kwa muda mrefu. Ni adhima ya Serikali kuhakiksha kwamba tunaondoa congestion katika maeno yote. Kwa hiyo, eneo lile na majengo ambayo yameshajengwa, hakika naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, inafaa kabisa kuwa Kituo cha Afya baada ya maboresho machache ambayo yataenda kukamilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, Mheshimiwa Mbunge pamoja na kwamba amesifia tunashukuru kwa hizo pongenzi kwamba Kituo cha Afya kimeshaanza kufanya kazi nzuri, lakini kinakosa baadhi ya wataalam. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azma ya Serikali kwamba yale majengo kwa maana ya vituo vya afya hatujengi ikawa kama picha. Tunataka wataalam wanaohusika ili upasuaji na shughuli zote zinazotakiwa kwenye kituo cha afya ziweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira. Wakati mwingine kuna watalam ambao ni lazima wawe trained. Kwa mfano, katika upasuaji lazima tuwe na wale watu ambao wanatoa dawa za usingizi na ndiyo maana tumewapeleka kuwa-train. Naamini na kituo hicho ambacho anakiongelea kitapata wataalam hao.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Halmashauri ya Mji wa Tarime, kata zote zilikuwa haina kituo cha afya bali walikuwa wanategemea Hospitali ya Mji. Tunashukuru tumepata Kituo cha Nkende ambacho kinaendelea kujengwa; lakini kuna kata nne za pembezoni ambazo zina zahanati tu, kwa maana ya Kata ya Kitale, Kata ya Kanyamanyori na Nanyandoto. Wananchi wa katia ya Kanyamanyori wameamua kuchangishana ili kuendeleza kile kituo cha afya kwa maana kujenga maternity ward na maabara:-

Ni lini sasa Serikali itawatia moyo wananchi wale kwa kutoa fedha kuweza kujenga kituo afya cha ili kupunguza vifo vya mama na watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kutembelea Jimbo la Mheshimiwa Mbunge na nikatembelea Hospitali ya Wilaya ambayo mwanzo ilikuwa inahudumia maeneo mengi sana kiasi kwamba kukawa kuna congestion kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge mwenyewe anakiri na anashukuru kwamba kimeanza kujengwa kituo cha afya na imebaki hizo kata ambazo yeye amezitaja. Naomba aendelee kuiamini Serikali kwamba kama ambavyo tumeanza kujenga katika hiyo kata kwa kadri bajeti itakavyoruhusu, tumeahidi tutatekeza na katika kata nyingine kwa jinsi bajeti itakavyokuwa inaruhusu.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika ziara ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI mwaka 2018 katika Jimbo la Monduli aliahidi kumalizia ujenzi wa Vituo vya Afya vya Nararami na Lemooti.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake kwa wananchi wa Monduli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama ambavyo katika swali lake ameuliza kwamba Mheshimiwa Waziri wa Nchi TAMISEMI aliahidi juu ya ujenzi kumalizia vituo vya afya viwili katika Jimbo lake, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hakuna hata siku moja ambayo Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais TAMISEMI alishawahi kuahidi akakosa kutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuvute subira. Kwa muungwana ahadi ni deni, nami nitamkumbusha kwamba kwa Mheshimiwa Kalanga uliahidi kumalizia vituo vya afya hivyo viwili. Kwa kadri fedha itakavyopatikana, hakika naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hivyo vituo viwili vya afya vitaweza kumaliziwa.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti,swali la kwanza, jokofu hilo la Hospitali ya Kinyonga halifanyi kazkwa sasa na Hospitali hii ya Kinyonga ipo sambamba kuelekea Mikoa ya Kusini. Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga jengo hilo kwa haraka sambamba na kuleta jokofu lenye uwezo la kuhifadhi zaidi ya mwili mmoja ili kuendana na chochote kinachoweza kutokea ili kukidhi haja hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali inampango gani kukarabati Kituo cha Afya Njinjo ambacho hali yake kwa sasa ni mbaya sana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Ngombale Vedasto,kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge, leo asubuhi kabla sijaingia hapa Bungeni nimefanya utaratibu wa kuwasiliana na Halmashauri na nina taarifa njema, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge leo tarehe 2 Mei, halmashauri inaingia mkataba na mdau wa Pan Africaambao wamekubali kujenga jengo la kisasa kwa ajili ya chumba cha kuhifadhia maiti, lakini kwa makubaliano kwamba na halmashauri nao watatununua jokofu la kisasa ili liweze kumudu hali ya uhitaji wa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaomba ukarabati waKituo cha Afya cha Njinjo, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba tunafanya ukarabati katika vituo vyote vya afya vile vile vilivyojengwa zamani, ili viwe na mwonekano wa sasa. Naye atakiri kwamba, katika nafasi aliyopata kutembelea vituo vya afya ambavyo tunavijenga sasa hivi tumevijenga vizuri, hali kadhalika hata hospitali za wilaya za zamani tungependa zikarabatiwe ziwe na muonekano wa kisasa kama kwa Hospitali ya Kilwa ya mwaka 1965, kwa vyovyote vile hata hali yake hailingani na hadhi ya hospitali ya Wilaya.
MHE. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutujengea Kituo cha Afya Hirbadawna kukarabati Kituo cha Afya cha Simbay, lakini ilituahidi kwamba itatusaidia kukamilisha Kituo cha Afya cha Bassotuna Endasak.Naomba jibu ili wananchi wa Hanang waweze kufurahi. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Dkt. Nagu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nipokee pongezi, yeye mwenyewe anakiri kwamba imefanyika kazi nzuri ya ukarabati wa vituo vya afya viwili kwake na ahadi yetu ya kukamilisha ukarabati wa ujenzi wa vituo vya afya kila kata iko pale pale.

Naomba Mheshimiwa Mbunge awaambie wananchi wawe na subira, lakini ni vizuri na wao wakaanza kujitokeza kwa zile kazi ambazo wanaweza kuanza kufanya ambavyo wananchi wake wamekuwa na mwitikio mkubwa waendelee kufanya na nasisi tutaunga mkono, lakini azma ni kuhakikisha kwamba hivyo vituo viwili navyo vinafanyiwa ukarabati.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Wananchi wa Bungu wanashida kubwa ya Kituo cha Afya na wenyewe walishaanza kujenga majengo. Je, Serikali ina mpango wa kuunga mkono Kata ile ya Bungu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kwenda Kibiti na tukaenda kutembelea mpaka Kituo cha Afya Mbwera, kituo cha afya ambacho kipo ndani kweli kweli unaenda delta kule, kama mtu anataka kuona jinsi ambavyo Serikali ya CCM inafanya kazi ni pamoja na kwenda maeneo kama delta, naomba nimhakikishie Mbunge na yeye mwenyewe ni shuhuda kazi nzuri ambayo inafanyika, hakika hata huko kituo cha afya ambacho hakijafanyiwa ukarabati kwa kadri fedha zitakazopatikana, tutaenda kukikarabati.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu hayo, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

(a) Kwa kuwa barabara hii ya Mtii – Mtae – Mnazi, kilometa 12.7 pamoja na Kwekanda – Hekcho – Rugulu hadi Mkomazi kilometa 17.5, zote hizi tumeziweka katika bajeti ya Mwaka wa Fedha 2019/2020 na bajeti tayari tumeshapitisha. Je, Serikali inatoa tamko gani kwa wananchi wa Mlalo?

(b) Kwa kuwa, barabara hizi siyo tu kwamba zinaunganisha Tarafa za Umba – Mlalo na Mtae, lakini pia zinaunganisha wilaya jirani za Korogwe na Same: Je, Serikali haioni kwamba kwa kutofanya wepesi wa kurekebisha barabara hizi inakuwa ni kikwazo kwa fursa za kiuchumi kwa wananchi wa Mlalo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kipekee kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Shangazi, amekuwa akipigia kelele sana kuhusu barabara hii ya kwenda Mtae na mara nyingi sana amefika ofisini kwetu. Naomba nimpongeze katika hilo.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake anaulizia kwamba tayari bajeti imeshapitishwa, nini tamko la Serikali kuhusiana na ujenzi wa barabara hiyo? Bajeti ambayo imepitishwa kwa ajili ya Wilaya ya Lushoto ni jumla ya shilingi bilioni 1.8. Kama katika bajeti yao na barabara hii ipo, ni vizuri wakahakikisha kwamba barabara hii ni muhimu ikaanza kutengenezwa mapema.

Mheshimiwa Spika, kwa vile bajeti inahusu shilingi bilioni 2.5 ambayo siyo rahisi, Bajeti ambayo imepitishwa ni
1.4 na wao wanahitaji shilingi bilioni 2.5; na kilometa katika Wilaya ya Lushoto ni jumla ya 935. Naomba Meneja wa TARURA ahakikishe katika vipaumbele vya barabara za kutengenezwa iwe pamoja na barabara hii.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, anaulizia je, Serikali haioni umuhimu wa kutengeneza barabara ya kuunganisha kwenda Lushoto na wilaya nyingine kwa maana ya fursa ya kiuchumi? Ni ukweli usiopingika kwamba maeneo ambayo barabara haipitiki tunakuwa tunawanyima wananchi fursa ya kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika pia kwamba bajeti yetu haiwezi ikakidhi kwa mara moja maeneo yote. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuvuta subira na yeye mwenyewe ni shuhuda, tangu tumeanzisha chombo cha TARURA kazi inayofanyika ni nzuri na hakika na barabara hii itawekwa kipaumbele ili iweze kutengenezwa.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya Ikola – Kasangantongwe imeharibika sana na mvua zilizonyesha na kusababisha wananchi kushindwa kutumia barabara hiyo na kuanza kutumia njia ya majini ambayo siyo salama.

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha kuijenga barabara hiyo ya Kasangantongwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) Mheshimiwa Spika, nimepata fursa ya kutembelea Jimbo la Mheshimiwa Kakoso na katika maeneo ambayo barabara zinajengwa unaona thamani ya pesa ni pamoja na Jimboni kwake. Yeye mwenyewe anakiri kwamba barabara hii ambayo anaitaja imeharibika kutokana na mvua ambazo zinanyesha na ni ukweli usiopingika kwamba katika maeneo ambayo mvua ni za uhakika ni pamoja na Jimboni kwake.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumwagiza Meneja wa TARURA ili akaangalie uharibifu wa hiyo barabara namna aone namna ambavyo anaweza angalau akafanya maboresho katika maeneo korofi sana ili barabara hii iweze kuendelea kupitika na wananchi waendelee kufaidi matunda ya CCM.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ni zaidi ya miaka 15 wananchi wa Segerea kupitia hiyo barabara ya Majumba Sita, Sitakishari wamekuwa wanapitia hiyo adha ya kukosa daraja, lakini ni kiungo kikubwa cha Gereza la Segerea, Seminari na sekondari mbalimbali: Je, Serikali haioni ni wakati sahihi wa kutengeneza hilo daraja ili kuondokana na hiyo adha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Changamoto ya madaraja katika kata mbalimbali za Jimbo la Segerea ni kubwa, nikianzia na Kata ya Tabata, Segerea, Kimanga na nyingine: Je, nini kauli ya Serikali kuondoa hii adha ukizingatia kwamba hili eneo letu halina barabara nyingi za lami na halina mitaro ili kuondoa adha inayowakabili wananchi wetu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kumbukumbu zangu naamini ziko sahihi kwamba ni mara ya tatu Mheshimiwa Anatropia anaulizia barabara hii. Naomba nichukue fursa hii kumpongeza kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi, changamoto ambayo tunakutana nayo kuhusiana na daraja hilo ni namna ambavyo mto unapanuka. Pia naomba yeye pamoja na Wabunge wote wanaotoka Dar es Salaam niwape maneno ya faraja kwamba ndani ya mwezi huu tumeweza kusaini kandarasi ya jumla ya shilingi bilioni 260 ambayo pia inashughulikia na adha ambayo inatokana na mafuriko mvua zinaponyesha na maeneo mengi ya Dar es Salaam yatakuwa yanafaidika katika hilo. Naamini hata hili suala la mto kupanuka baada ya kwamba kingo zimejengwa, adha itapungua.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali maana yeye mwenyewe anashuhudia jitihada zinafanyika.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, ameongelea madaraja mengi. Naamini katika package ya shilingi bilioni 260 nayo itakuwa imekuwa covered. Kama haitoshi, tumeweza kuweka taa 5,000 ndani ya Mji wa Dar es Salaam kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanaendelea kufaidi matunda ya chama chao.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, pamoja na marekebisho ambayo yamefanyika, ni kwamba sasa ule moshi zamani ulikuwa unafika mbali, baada ya marekebisho ule moshi bado unatoka na bado unaathiri wananchi waliokuwa jirani, unasababisha watu kukohoa na harufu chafu kwa wananchi wanaozunguka lile eneo. Swali langu: Je, Serikali ilishafanya utafiti kwa sababu watu wanakohoa, tumejua ni madhara gani ya kiafya yanayosababishwa na moshi huo?

Swali langu la pili; ni kwa nini sasa NEMC wasirudi tena kule Dundani na kuhakikisha kwamba ule moshi unatafutiwa namna ambayo itaudhibiti usiendelee kuchafua mazingira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nikiri kwamba Mheshimiwa Ruth Mollel ni Diwani wa kata husika, kwa hiyo, yeye ni mdau katika eneo hilo. Kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi, kwamba mpaka sasa hivi hakuna taarifa ambayo imekuja Ofisi ya Mkurugenzi ikionesha kwamba kuna kasoro ambazo Serikali inatakiwa irekebishe, naomba Mheshimiwa Mbunge kwa kutumia vikao vyake alipeleke hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa sababu sisi tunajali afya ya mwananchi kuliko jambo lingine lolote, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, pamoja na swali lake la pili kwamba angetaka NEMC waende kwa mara ya pili kutazama; kwa sababu mtaji wetu kwa mwananchi ni kuhakikisha kwamba ana afya bora, basi naomba nimhakikishie kwamba Serikali kwa kupitia NEMC tutakwenda kuchunguza na tujiridhishe pasi na mashaka kwamba hakuna madhara ambayo yanatokana na kichomea taka hiki.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa madawa yaliyokwisha muda wake (expired drugs) ni hatari sana katika maisha ya binadamu; na kwa kuwa baadhi ya maduka hayakaguliwi vizuri kuhakikisha kwamba madawa yaliyokwisha muda hayapo.

Je, Mheshimiwa Waziri anasemaje kuhusu ukaguzi wa maduka yote ambayo yana madawa hayo yaliyokwisha muda wake?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taratibu zetu za afya, dawa zilizoisha muda au matumizi hazipaswi kutumika kwa matumizi ya binadamu. Mahospitali pamoja na wauzaji wa maduka binafsi wanatakiwa wazitenge tofauti na dawa ambazo zinaendelea kutumika ndani ya vituo vyetu vya kutolea huduma za afya lakini vilevile katika matumizi ya dawa za kuuzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna utaratibu maalum ambao umewekwa ambapo dawa na vifaa vya hospitali havichomwi tu kama takataka nyingine, vina utaratibu wake na utaratibu huu upo. Nitoe rai tu kuhakikisha kwamba mamlaka ambazo zinasimamia ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya TFDA na Baraza la Famasia, basi wapite kuhakikisha kwamba wanatoa elimu hiyo na kuweka utaratibu mzuri wa uteketezaji wa hizi dawa ili zisije zikaingia katika mikono isiyo salama.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Waziri yenye kutia moyo lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali ina mpango wa kukarabati Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya na kutoa vifaatiba. Je, ni lini sasa itatoa X-ray mashine katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto ili kupunguza msongamano au usumbufu wa wananchi wangu kutoka Lushoto kwenda mpaka Tanga hadi Muhimbili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Jimbo la Lushoto lina Kata 15 na Kituo cha Afya kimoja tu. Wananchi wa Kata za Gare na Ngwelo kwa nguvu zao wenyewe wameanza kujenga maboma hayo ya Vituo vya Afya. Je Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha au wa kuwapatia fedha zile ambazo zinatolewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kujenga vituo hivyo? Nia na madhumuni ni kupunguza msongamano mkubwa uliopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza juu ya uwepo wa X-ray, naomba nimtoa wasiwasi Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Lushoto kwamba mchakato uko kwenye hatua za mwisho kupitia MSD. Muda si mrefu X-ray ile itapatikana ili wananchi wa Lushoto na maeneo ya jirani waweze kupata huduma ya vipimo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika swali lake la pili, naomba nimpongeze yeye mwenyewe na Mheshimiwa Shangazi wamekuwa wakifuatilia sana kuhusiana na Hospitali ya Lushoto. Naomba pia niwapongeze wananchi ambao wameanza ujenzi wa Kituo cha Afya. Hakika pale ambapo wananchi wanaanza Serikali inawaunga mkono mara moja. Naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwa kadri bajeti itakavyoruhusu na fedha ikipatikana tunahakikisha tunapeleka maeneo ambayo tayari nguvu ya wananchi ilishakuwepo. Mchakato utakavyokamilika hakika hatutawasahau wananchi wa eneo alilolitaja.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hospitali ya Wilaya ya Mji wa Tarime ambayo kiukweli inatoa huduma kama Hospitali ya Wilaya au ya Mkoa naweza nikasema na Kanda Maalum Tarime Rorya, Mheshimiwa Naibu Waziri alitembelea na akaona ni jinsi gani inaelemewa kwa utoaji wa huduma. Hivi ninavyoongea chumba cha kuhifadhia maiti kwa maana ya mortuary kwanza ni kifinyu lakini pia mashine yake kwa maana ya compressor haifanyi kazi na wale ndugu zetu ambao tunawahifadhi pale wakikaa muda mdogo wanaharibika. Nataka kujua commitment ya Serikali ya kuhakikisha kwamba inasaidia ukarabati au upanuzi wa mortuary ikiwemo kusaidia hiyo mashine ya compressor kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Tarime haina kipato cha kutosha. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge nilipata fursa ya kutembelea hospitali ile ambayo ina congestion kubwa na bahati nzuri nilipata fursa nikiambata na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Maelekezo ambayo yalikuwa yametolewa, kwanza ni kuhakikisha kwamba dawa za kutosha zinatolewa ili kukidhi haja kwa sababu wananchi ni wengi wanaopata huduma pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili ambalo amelisema kuhusiana na chumba hicho cha kuhifadhia maiti ambacho mashine imeharibika kiasi kwamba sasa mwili unaharibika ndani ya muda mfupi, naomba seriously tukitoka hapa tuwasiliane na Mheshimiwa Mbunge ili tuone hatua za haraka za kuchukua kuhakikisha kwamba mochwari ile inafanya kazi.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali madogo ya nyongeza. Swali la kwanza ni kwamba Wilaya ya Mbogwe ni Wilaya mpya na katika Mkoa wa Geita, ni Wilaya pekee ambayo kwa kweli ina watumishi wachache sana wa Idara ya Afya: Je, Serikali ina mpango gani wa kutuongezea watumishi hao?

Swali la pili ni kwamba Serikali imejitahidi kutupatia vituo viwili vya afya na huduma mojawapo ni ya mortuary; lakini kuna shida ya mortuary cabinets, yale mafriji ya kuhifadhia maiti hayajaletwa na watu MSD. Sasa Serikali ina mpango gani kupitia MSD kutuletea hiyo huduma mara moja? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza Mheshimiwa Masele anaongelea upungufu wa watumishi wa Kada ya Afya katika Wilaya yake ambayo ni miongoni mwa Wilaya mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika na wewe umekuwa shuhuda kwamba wakati mwingi zinapoanzishwa Halmashauri mpya kumekuwa na nakutopata watumishi wa kutosha. Kwa hiyo, naomba kwanza niagize Ofisi ya RAS wahakikishe kwanza ndani ya Mkoa watazame ikama ilivyo ili katika maeneo ambayo yana upungufu mkubwa kama eneo la Mheshimiwa Mbunge waweze ku-balance.

Mheshimiwa Spika, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati nafasi nyingine zikitoka kwa ajili ya kuajiri, tutahakikisha kwamba tunazingatia maeneo yenye upungufu ikiwa ni pamoja na eneo lake kuwapeleka watumishi wale.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni juu ya kupatikana kwa friji kwa ajili ya kutunza maiti. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni azima ya Serikali kuhakikisha maeneo yote ambayo mortuary zimejengwa, friji zinapelekwa. Naomba tuwasilaine na Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi cha maswali na majibu ili tujue MSD lini watapeleka hayo masanduku.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niliulize swali dogo la nyongeza. Hospitali ya Nyamiaga ni Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Ngara ambayo ilipatiwa hadhi kutoka kituo cha afya mwaka 2013, lakini mpaka sasa hivi hakuna maboresho ya miundombinu katika hospitali hiyo. Kwa hiyo kuna upungufu wa jengo la utawala, jengo la upasuaji, jengo la X-Ray, mortuary na labor Ward:-

Ni lini Serikali itaweza kutenga fedha kwa ajili kuboresha hospitali hiyo ukizingatia kwamba hatuna hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa
Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gashaza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba maeneo mengi ambayo vilikuwa aidha vituo vya afya au ilikuwa zahanati ikapandihswa hadhi; kwanza tumekuwa na changamoto ya eneo, hata pale ambapo tumepandisha hadhi kituo cha afya kuwa hospitali ya Wilaya inakuwa haina hadhi ya kulingana na hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali katika utaratibu mziwa wa kuboresha na kujenga Hospitali za Wilaya zile za mwanzo zinaanza kuonekana kwamba zimeanza kuwa outdated. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kadri ambavyo tumeanza na hosptali 67, zikaongezeka 27 kwa kadri bajeti itakavyoruhusu hakika na wao hatutawasahau ili wale na Hosptali ya Wilaya yenye hadhi ya kulingana na Hospitali za Wilaya za Halmashauri nyingine.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa ujenzi wa Kituo cha Afya Mbori ambacho hata wewe unakifahamu, Waziri wa TAMISEMI anakifahamu, sasa ni zaidi ya miaka kumi kinajengwa kwa nguvu za wananchi na Halmashauri ambayo haina fedha; na kwa kuwa nimeomba shilingi milioni 500 TAMISEMI wasaidie kukamilisha jengo lile:-

Je, TAMISEMI au Serikali inasemaje kuhusu kukamilisha Kituo cha Afya Mbori?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kama kuna Waheshimiwa Wabunge ambao wamekuwa wakiongelea kituo cha afya kwa kurudia mara nyingi ni pamoja na Mheshimiwa Lubeleje; na hivi karibuni alipata fursa ya kuonana na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na akamhakikishia.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumepata fedha kiasi, tumepeleka kwenye hospitali na vituo vya afya ikiwa ni pamoja na Kongwa shilingi milioni 400. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Lubeleje, ahadi ya Mheshimiwa Waziri hakika atatekeleza kama alivyomwahidi. Naomba avute subira fedha yoyote ikipatikana hatumsahau Mheshimiwa Lubeleje.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuweza kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha ya Serikali. Lakini Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba mmeelekeza ile asilimia 15 ya mapato kutoka kwenye hospitali na vituo vya afya ziende kulipa on call allowance kwa madaktari hawa, lakini bado kuna changamoto kwa sababu kuna halmashauri ambazo ni nyingi zina mapato madogo sana.

Sasa je, nyie kama Wizara mmejipangaje kuhakikisha kwamba zile halmashauri ambazo mapato yake ni madogo mtumie njia gani nyingine ambayo itakuwa muafaka ili kuweza kuhakikisha kwamba madaktari hawa wanapata stahiki zao?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa bado kumekuwa na changamoto za kupandishwa vyeo kwa mfano kutoka clinical officer kwenda kuwa daktari lakini vile vile kutoka mkunga kwenda kuwa muuguzi na vile vile promotion zao bado tumeziona zikiwa zina suasua. Je, nyie kama Wizara mmejipanga vipi kuhakikisha kwamba mnatatua changamoto hii pia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kwanza naomba uniruhusu kipekee nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Neema, amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba wananchi wa Mkoa wa Njombe wanapata huduma nzuri ya afya. Binafsi ameonekana akichangia mifuko ya saruji lakini pia nikimuona amepeleka mashuka kwa ajili ya kusaidia wagonjwa wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo, katika swali lake la kwanza anaongelea namna ambavyo uwezekano mdogo kwa baadhi ya halmashauri. Kwanza katika kuimarisha tumeajiri wahasibu zaidi ya 350 ambao katika vituo vya afya wameenda kusimamia na mapato yameongezeka. Hakika fedha hii ikiweza kusimamiwa vizuri hakuna uwezekano wa kwamba madaktari na wauguzi wanaweza wasilipwe on call allowance. Nilienda kituo cha afya Kisosora pale Tanga nimekuta katika fedha ambazo zinapatikana mpaka wanafanya na ukarabati katika vituo vya afya. Kwa hiyo, ni suala tu la kusimamia vizuri na hakika maeneo yote ambayo yanasimamiwa vizuri, fedha inatosha na hatujapata malalamiko hivi karibuni.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anaongelea suala zima la kuwapandisha vyeo. Hizi n afasi zinategemeana na ujuzi kwa hiyo si rahisi kwamba mtu atapanda bila kwenda kuongeza ujuzi na ni matarajio ya Mheshimiwa Mbunge kwamba asingependa akapandishwa cheo mtu ambaye hana ujuzi mahsusi na ndiyo maana zimekuwa zikitolewa fursa za wao kujiendeleza na pale anapojiendeleza na kuhitimu akirudi huwa anapandishwa cheo.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa matatizo ya daraja la Segerea ni ya muda mrefu sana na kila wakati liko katika upembuzi yakinifu; na kwa kuwa Serikali sasa inataka kufanya tena usanifu kupitia TARURA; mimi nauliza swali: Je, kwa nini TARURA sasa wasianze kujenga hilo daraja la Segerea badala ya kuanza tena upembuzi yakinifu ili kuwasaidia wananchi wa Segerea ambao wanapata shida sana kutokana na ukosefu wa daraja lile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa matatizo wanayopata wananchi wa Segerea yanafanana kabisa na yale wanayowapata watu wa Jangwani pale maeneo ya Magomeni: Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha daraja la Jangwani ili kuondoa matatizo ya kufunga barabara ile wakati wa mvua nyingi kila wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi maswali yote mawili yanafanana. Adha ambayo tunaipata kutokana na lile daraja ambalo mto unahama, lakini na swali lake la pili kuhusiana na daraja la Jangwani ambalo linajaa maji kila muda, naomba Mheshimiwa Mbunge arejee katika siku moja ambayo nilijibu hapa, kwamba jumla ya shilingi bilioni 260 zimetengwa kwa ajili ya kuanza usanifu na kuhakikisha kwamba tunapata suluhu ya kudumu kuhusiana na Mto Msimbazi. Pia akubaliane name, kama ambavyo tunaweza tukafanya makosa tukajenga hilo daraja, baada ya muda likawa linaendelea kujaa, ndiyo maana tumemwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira kama ambavyo nimetoa majibu katika jibu langu la msingi, kwamba ni vizuri tukafanya usanifu wa kina kujua hasa tatizo ili ujenzi ukikamilika tuwe tumepata suluhu ya kudumu.
MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Kwa kuwa swali la msingi linahusu muunganiko wa daraja na barabara; na kwa kuwa sote tumeshuhudia kwa macho au kupitia vyombo vya habari jinsi Mji wa Dar es Salaam ulivyoharibika kwa mafuriko; na kwa kuwa ujenzi wa madaraja na barabara umechangia kuhakikisha kwamba usafiri umekuwa siyo mzuri kwa watoto wetu, kwa watu wazima na kwa wagonjwa kutokana na mafuriko yaliyokuwepo: Je, Serikali itachukua hatua gani za dharura kuhakikisha mafuriko hayo hayataendelea tena na hayatatokea; na kuhakikisha Mji wa Dar es Salaam unarudi kama ulivyokuwa hapo awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sisi sote ni mashuhuda kwamba mvua ambazo zinanyesha Dar es Salaam sasa hivi ni nyingi sana ambazo hatukuzitarajia. Kwa hiyo, kwanza ni sisi wote kushiriki kuhakikisha kwamba tunapambana na tabianchi ambayo inaleta mwongezeko wa mvua ambazo hatuwezi kuzitarajia. Sasa tunafanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kipekee nichukue fursa hii kupongeza UDART jinsi ambavyo wamekuwa wakipambana na hali hii pale ambapo maji yanakuwa yamezidi, tunalazimika kusimamisha usafiri ili kusije kukawa na madhara makubwa, lakini immediately zinafanyika juhudi za kuhakikisha maji yale yanaondolewa na usafiri unarejea kama kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge, ni ukweli usiopongika, kwa mvua ambazo zinanyesha sasa hivi; na bahati nzuri watabiri wa hali ya hewa walitufahamisha kwamba mvua zinatarajiwa kunyesha nyingi sana, kwa hiyo, hakuna namna ambavyo tunaweza tukasema tutafanya kuzuia mvua kwa sababu ni calamity ambayo inaweza ikatokea muda wowote. Kwa hiyo, tuwe na subira, hali ya Dar es Salaam itarudia katika hali yake baada ya mvua hizi kukoma kama ambavyo wametuambia.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunpa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Kule Moshi Vijijini kwa asili kabisa hali ni mbaya sana wakati wa mvua kwa sababu ya aina ya udongo ambao uko kule, lakini hali ni mbaya zaidi katika Kata ya Arusha chini kule TPC katika kijiji cha Chemchem ambacho kimetengwa na Mto Kikavu ambao wakati wa mvua kunakuwa hakuna mawasiliano kabisa na sehemu nyingine zozote za Jimbo.

Mhshimiwa Mwenyekiti, toka mwaka 2012, daraja hilo la Chemchem la hapo kwenye kivuko cha Mto Kikavu limekuwa likitengewa fedha, lakini ujenzi mpaka kesho haujaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri, ni lini mtakuja kuwaunganisha watu wa Chemchem na wenzao wa huku Tanzania?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kijiji ambacho Mheshimiwa Mbunge anakitaja kwangu mimi ndiyo nakisikia. Katika swali la msingi sikutarajia swali la kutoka huko ambako Mheshimiwa Komu anasema. Ni vizuri sasa nimwambie Mheshimiwa Mbunge, baada ya kipindi hiki cha maswali na majibu ni vizuri tukawasiliana tujue uhalisia ukoje ili tuweze kutatua tatizo ambalo lipo.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwe Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba niongeze swali dogo la nyongeza, kwamba kule kwangu kuna barabara ya kutoka Waama mpaka Masusu na hatimaye mpaka kule Lalaji na barabara nyingine ya Maskaroda na kwenda Lambo na kwenda Dareda ambapo zinaunganisha wananchi na hospitali na nilishatoa ombi: Je, Serikali inasemaje ili kunisaidia na watu wale ambao wana kilomita 20 kwenda kwenye hospitali wapate namna ya kufika? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kwenda Jimboni kwa Mheshimiwa Dkt. Nagu kutatua mgogoro wa kijiji na tukafanikiwa kuutatua mgogoro ule. Ingekuwa vizuri sana Mheshimiwa Nagu kama ungeniambia tukapata na fursa ya kwenda kutembelea huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba huduma ya usafiri na hasa kwenda hospitali kama ambavyo yeye amesema kwenye swali lake, ni vizuri tukawasiliana na Meneja wa TARURA tujue nini hasa ambacho kinatakiwa kifanyike ili wananchi wetu waendelee kupata huduma na hasa ya kwenda hospitali.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini pia niipongeze Serikali kwa kutuletea fedha hizo shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya unaoendelea hivi sasa, lakini pamoja na majibu haya mazuri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwanza kabisa kuna msongamano mkubwa bado katika Kituo hiki cha Afya cha Dongobesh kwa sababu ya huduma ambayo si nzuri sana kwenye zahanati zetu. Je, ni nini kauli ya Serikali wakati tukisubiri kukamilika kwa ujenzi ambao ndio kwanza umeanza wa Hospitali ya Wilaya ambao utapunguza msongamano kwenye kituo hicho cha afya kupeleka huduma ya vifaa tiba pamoja na watumishi kwenye zahanati zinazozunguka Kituo hiki cha Afya cha Dongobesh?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Tarafa ya Yaeda Chini haina kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itapeleka Kituo cha Afya katika tarafa ya Yaeda Chini ambayo mioundombinu yake migumu na huko ndiko wanakoishi wenzetu Wahadzabe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Ester Mahawe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, tupokee pongezi za kutoka kwa Mheshimiwa Esther. Nilipata fursa ya kwenda Kituo cha Afya Dongobesh na pia nikapata fursa ya kushiriki kuzindua ujenzi wa Hospitali ya Dongobesh kwa maana ya Hospitali ya Wilaya. Kipekee naomba nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Mahawe pamoja na Mheshimiwa Flatey Massay kwa ushirikiano mkubwa pamoja na wananchi wao katika kuhakikisha kwamba, huduma za afya zinaboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake anaongelea juu ya suala zima la kupeleka watumishi katika zahanati ili kusiwe na msongamano. Wewe ni shuhuda. Katika mwaka wa fedha 2019/2020, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumepeleka maombi ya ajira elfu 15 kwa ajili ya watumishi wa Kada ya Afya kwa kadri kibali kitakavyopatikana, naomba nimhakikishie Mbunge na huko nako hatutawaacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, anaongelea juu ya suala zima la kujenga Kituo cha Afya katika Tarafa ya jirani ambako wanaishi jamii ya Wahadzabe ambao wanauhitaji mkubwa. Naomba aendelee kuiamini Serikali tumeahidi tunatekeleza na naamini na yeye anaridhika na mwendo ambao tunaufanya katika kujenga vituo vya afya.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri amefika na Serikali imetupa fedha ya kujenga hospitali ya wilaya, lakini Mheshimiwa Waziri atakumbuka tulimsimika kama Mzee wa Mbulu Vijijini na akatuahidi atatupatia Kituo cha Afya kile cha Maretadu na maombi yako kwake. Ndugu yangu awaambie watu wa Maretadu je, kituo cha afya kitaletewa fedha lini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muungwana ahadi ni deni. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali kama ambavyo tumepeleka fedha katika Kituo cha kwanza cha Dongobesh, tukapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya, halikadhalika tutahakikisha kwamba, pale nafasi inapopatikana hatutasahau kwa sababu tumeahidi.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Mgombezi ina zahanati na Kata ya Mtonga ina zahanati ambayo ina wakazi wengi, hasa ikizingatiwa kwamba, kuna mashamba ya mkonge. Je, watakuwa tayari sasa kutusaidia kupandisha hadhi Zahanati ya Mtonga pamoja na Zahanati ya Mgombezi ili viwe vituo vya afya, hasa ikizingatiwa kwamba, kuna watu wengi sana ambao wana shughuli za mkonge kule? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mary Chatanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba, tunajenga vituo vya afya vyenye ramani na hadhi ya kufanana na vituo vya afya. Pale ambapo zahanati ambayo imejengwa ina hadhi ya kulingana na vituo vya afya hatusiti kufanya hivyo, lakini tunafanya kwa kuzingatia kwamba, ramani ile ambayo vituo vya afya vinajengwa na zahanati hiyo ifanane na ramani hizo, lakini pia hata ukubwa wa eneo; inahitaji eneo lisilopungua ekari 15 kuwa na kituo cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sina uhakika katika zahanati ambazo Mheshimiwa Mbunge anaongelea zina maeneo na ramani ya kufanana na vituo vyetu vya afya? Tutafanya vile baada ya kujiridhisha kwamba, vigezo vyote vimetosheleza, kama ambavyo kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama kuna zahanati ambazo tumezipandisha hadhi kuwa vituo vya afya baada ya kuridhika kwamba, matakwa yote ya kituo cha afya yanakamilishwa.
MHE. OMARI M. KIGUA: Ahsante Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kabisa nami naungana na Serikali kwamba kuna umuhimu wa Serikali kushirikiana na sekta binafsi katika kuwaletea Watanzania huduma. Pamoja na hali hiyo, zimejitokeza changamoto nyingi sana sana katika Hospitali hii ya KKKT mojawapo ni suala la utawala.

Swali: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari sasa kuangalia utaratibu ulio mzuri ili dhana hasa ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi iweze kufikiwa?

Swali la pili, kwa kuwa Kilindi haina Hospitali ya Wilaya: Je, Serikali iko tayari sasa kuitengea fedha Wilaya ya Kilindi ili iweze kupata Hospitali ya Wilaya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma na lengo la Serikali kuhakikisha kwamba zile hospitali ambazo tunashirikiana katika kutoa huduma kwa maana ya DDH, suala la utawala bora inakuwa ni kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawe ni shuhuda kwamba katika swali lake amesema kuna tatizo la utawala. Sasa ni vizuri Mheshimiwa Kigua tukitoka hapa tuelekezane hasa tatizo ni nini ili tuweze kutoa ufumbuzi ili wafanyakazi nao waweze kuona ni sawa na ambavyo wanafanya katika hospitali zetu za Wilaya. Kwa sababu suala la kuwa na utawala bora ni jambo la msingi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kigua atakubaliana na Serikali kwamba azma ya kuhakikisha kwamba hospitali zinajengwa katika maeneo yote ambayo Halmashauri hazina Hospitali za Wilaya inafikiwa. Kwa kuanzia, yeye mwenyewe ni shuhuda, katika bajeti ambayo Bunge lako Tukufu limetupitishia, tumeweza kuwatengea kwa kuanzia shilingi milioni 200 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Msente. Naamini baada ya kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa hospitali 67 tulizoanza nazo na 52, hakika naomba nimtoe shaka kwamba na Kilindi tutakwenda.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri yenye matumaini hasa kwa mwaka huu kutengewa hizo shilingi milioni 34, lakini hii barabara ya Kidiwa - Tandali imeshafanyiwa upembuzi yakinifu, ingawa sasa hizo fedha zitatafutwa mpaka lini? Hapo sasa napenda kufahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba Tarafa ya Mgeta kama alivyotembelea miaka ya nyuma, landscape yake bado ni ile ile ya milimani na watu wanaishi milimani. Kwa sasa tunategemea barabara hii kubwa moja toka Sangasanga kwenda mpaka Nyandila - Kikeo. Barabara hii ni mbovu sana hasa wakati wa masika; na tulishaahidiwa. Nakumbuka miaka ya 1970s alipokuja Mheshimiwa Abdu Jumbe aliahidi kwamba tutatengenezewa kwa kiwango cha lami. Ni kweli naweza nikalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete alipokuja aliahidi kwamba barabara hii itatengenezwa kwa kiwango cha lami kulingana na ubovu wake na nauli inakuwa kubwa: Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kujenga barabara hii ya Sangasanga mpaka Nyandila kwa kiwango cha lami?

Swali la pili. Katika kutatua changamoto za usafiri katika Tarafa hii ya Mgeta, wananchi wamejitolea kutengeneza barabara nyembamba za kupita pikipiki, lakini wanakutana na changamoto ya utaalamu; wakati mwingine hawajui barabara iende hivi, kwa hiyo, wanakutana na changamoto hizo, lakini pia wanakutana na changamoto sehemu nyingine inabidi ijengwe madaraja au karavati.

Je, Serikali sasa iko tayari kuungana na wananchi hawa wa Tarafa ya Mgeta ili kupeleka wataalam pamoja na kuwajengea madaraja ili tuweze pia kutumia usafiri wa pikipiki kuunganisha vijiji na Kata? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, machozi tuliyoshuhudia yakitoka kwa Mheshimiwa Mbunge wa Mlimba pale, yanatosha kwa Mkoa wa Morogoro. Kwa hiyo, isingependeza tukapata machozi mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Dkt. Tisekwa akubaliane nami kwamba ahadi zote zinazotolewa na Viongozi Wakuu kwa maana ya Marais, hata kama Rais aliyetangulia ndio aliyetoa ahadi, sisi kama Serikali, ahadi hizo tunazitunza na ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba ahadi za viongozi wetu tunazitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Mheshimiwa Mbunge atakuwa shuhuda, katika ahadi ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, katika bajeti ambayo tumepitisha, tumeanza kutekeleza katika maeneo yote ambayo ahadi zimetolewa. Tumeanza kujenga lami kwa kilometa moja moja. Kwa muungwana ahadi ni deni, naomba nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, tutatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili suala la pili ambapo wananchi wameanza kutengeneza barabara kwa ajili ya kupita angalau kwa pikipiki, lakini kinachokosekana ni utaalam, naomba nichukue fursa hii kumwagiza coordinator wa Mkoa wa Morogoro ahakikishe kwamba anamwagiza Meneja wa Wilaya husika ili kwenda kutoa utaalam ili wananchi pale ambapo wanatoa nguvu yao isije ikapotea na aone namna ambavyo na Serikali tunaweza tuka- complement ili kazi nzuri iweze kuonekana.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Kama ilivyo kwenye swali la msingi, kule Moshi Vijijini katika Kata ya Mabogini iko barabara inayotoka Mabogini inakwenda Chekereni mpaka Kahe. Ile barabara huwa inakarabatiwa na wananchi na wakati mwingine na TARURA lakini kwa fedha kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliwahi kuuliza swali la msingi hapa, nikaahidiwa kwamba TARURA inao mpango mkubwa wa kuifanyia kazi hiyo barabara ili iweze kupitika katika kipindi chote cha mwaka. Sasa hivi tunavyoongea, ile barabara haipitiki kabisa kwa sababu imebadilika kuwa mfereji. Naomba …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Komu, uliza swali tafadhali.

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumwuliza Naibu Waziri, ni lini hiyo kazi ya kuitengeneza hiyo barabara itaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni jana tu Mheshimiwa Komu aliuliza swali kuhusiana na barabara ya Jimboni kwake na tukakubaliana kwamba ni vizuri tukaenda kwenye uhalisia. Naamini na hili anaongezea ili wakati tutakavyokuwa tunaenda Moshi tukashughulikie barabara zote mbili, tukitizama tujue suluhu ipi ambayo inatakiwa? Tujue tukiwa site. Mheshimiwa Komu, naomba niipokee katika lile la jana na la leo, kwa hiyo, tunakuwa na barabara mbili.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo lililopo kwenye Tarafa ya Mgeta linafanana kabisa na tatizo lililopo kwenye katika Tarafa ya Namasakata, katika Jimbo la Tunduru Kusini. Barabara ya Chemchem - Ligoma inazaidi ya miaka 10 tangu 2007 haijawahi kutengenezwa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ile ili wananchi waweze kufaidika na Uongozi wa Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge ni mashuhuda kwamba tangu tulivyoanzisha chombo chetu kwa maana ya TARURA, wengi wamekuwa wakipongeza ufanisi ambao umetokana na chombo hiki. Kwa hiyo, ni vizuri sasa tusiishi kwa historia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwmaba ni vizuri tukawasiliana na Meneja wa TARURA ili atupe uhalisia katika barabara hii ambayo anaongelea na hiyo miaka 10 ambayo iliahidiwa, hakika kwa Serikali ya Awamu ya Tano tunaahidi na kutekeleza.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nipate kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa suala la ultrasound katika vituo vya afya au Hospitali za Wilaya na Halmashauri, ni suala kubwa sana na halipatikani maeneo mengi nchini Tanzania na hii inaathiri kina mama na wanaokwenda katika Hospitali hizo kuangalia hali zao za kiafya hasa katika suala la tumbo.

Je, ni lini sasa Serikali itaweka mkakati kupeleka ultrasound kwenye vituo vyote vya afya nchini Tanzania na Hospitali za Wilaya ili wanawake wapate huduma hizo katika hospitali nchini?

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Mlimba, Kituo cha Afya cha Mlimba kina ultrasound na mfuko wa Jimbo nilichukua nafasi mimi kumpeleka kwa kuomba na DMO kwenda kumsomesha mtaalam ambaye amesharudi na huduma hii inapatikana Kituo cha Afya cha Mlimba, lakini kuna Kituo cha Afya cha Mchombe, hakina ultrasound.

Je, nini kauli ya Serikali kupeleka ultrasound katika Kituo cha Afya cha Mchombe, ndani ya Jimbo la Mlimba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nakubaliana kabisa na Serikali inatambua umuhimu wa uwepo wa kifaa cha ultrasound na ndiyo maana katika vituo vyote vya afya ambavyo tunavijenga, tayari fedha tulishapeleka MSD kwa ajili ya kuhakikisha kwamba kituo cha afya vinavyokamilika vinakuwa na vifaa ikiwa pamoja na ultrasound.

Mheshimiwa Spika, na kwa mfano, katika swali la msingi la Kituo cha Afya cha Ujiji, tayari fedha imepelekwa na fedha hiyo imepelekwa tarehe 29 Aprili uliopita na baada ya wiki tatu, katikati ya mwezi Juni, tayari ultrasound itakuwa imefika.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili, hicho kituo cha afya ambacho anakisema cha Mchome, naamini ni miongoni mwa vituo vya afya ambavyo tayari tumeshapeleka fedha MSD, kwa hiyo, tukishamaliza kipindi cha maswali na majibu, ni vizuri tukakutana na Mheshimiwa Mbunge ili tutazame wao lini wanatarajia kupata ultrasound.
MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi, Kituo cha Afya cha Pasua kilichopo Manispaa ya Moshi nacho kina tatizo la ultrasound, lakini pamoja na mortuary. Je, ni lini Serikali itapeleka ultrasound na kujenga hicho chumba cha kuhifadhindugu zetu waliotangulia mbele ya haki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu katika swali la msingi, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo vituo vya afya vinajengwa, vinakuwa ni vituo vya afya ambavyo vinakamilika kwa maana ya kuwa na watalaamu lakini pia kuwa na vifaa vya kutosha.

Mheshimiwa Spika, sasa katika swali lake anaongelea Kituo cha Afya ambacho kinaitwa Pasua kiko Moshi na anasema kuna haja ya kuwepo mortuary lakini pia na uwepo wa ultrasound. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hakuna kituo cha afya hata kimoja ambacho tungependa kikawa kituo cha afya nusu, tungependa vituo vya afya vyote vikamilike, ni vizuri tukaelezana tatizo ni nini na hasa ukizingatia kwamba, hata kwa Halmashauri ya Moshi, mapato yake ya ndani yapo ya kutosha kabisa. Kwa hiyo, ni suala tu la mipango tujue nini kifanyike kwa haraka ili wananchi waweze kupata huduma hizo.
MHE. OMARI A. KIGODA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza Bunge lililopita niliuliza kuhusu suala la ambulance na Mheshimiwa Waziri aliniambia tuendelee kutumia magari ya kawaida mpaka ambulance itakapopatikana. Tatizo la magari ya kawaida hayana vifaa maalum vya huduma ya kwanza kwa hiyo wagonjwa wengi wanaotoka pale hospitali kwenda hospitali nyingine wengi wanapoteza maisha njiani. Sasa nauliza tena, je, ni lini tena Serikali itaona umuhimu wa kuipatia Hospitali ya Handeni ambulance, asante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu kipekee kabisa nitumie fursa hii kuwapongeza Wabunge wa Mkoa wa Tanga maana maswali ya kuhusiana na afya wiki hii yamekuwa kila leo yakiulizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake ambalo anauliza juu ya umuhimu wa Serikali kuhakikisha kwamba inapatikana ambulance kama ambavyo tulishawahi kujibu hapa, naomba niendelee kumsihi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kwa kupitia Wizara ya Afya ipo kwenye mchakato katika hatua za mwisho kuhakikisha kwamba ambulance zinanunuliwa. Na naamini katika maeneo ambayo yatakumbukwa kuhakikisha kwamba kile tulichoahidi kama Serikali tunatekeleza na yeye atapata.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Lupembe Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ina vituo vinne na kimoja kipo kwenye ujenzi lakini vituo vyote hivi havina vifaa muhimu kama vile Ultra sound na X-ray machines pamoja na kwamba tunatoa huduma ya upasuaji katika Kituo cha Lupembe.

Je, ni lini Serikali italeta vifaa hivi muhimu sana kwa ajili ya kuwasaidia wananchi waweze kupima baadhi ya vipimo kwenye hivi vituo vya afya? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hongoli, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kabisa, kama kuna Wabunge ambao wanafuatilia masuala ya afya kwenye majimbo yao, ni pamoja na Mheshimiwa Hongoli na hivi karibuni alikuja ofisini na tukakubaliana. Amepata fursa ya Kituo cha Afya cha Kichiwa kinajengwa na naomba uniruhusu, ifike mahali nitaleta orodha ya jinsi ambavyo Serikali imefanya commitment na fedha ambazo tumeshalipa MSD, kinachosubiriwa ni vifaa kupelekwa. Kama ambavyo nimekuwa nikijibu kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha vituo vya afya vyote ambavyo vinajengwa vinapatiwa vifaa ili vitumike kama ambavyo tumekusudia.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa ya Moshi ilishaleta ombi Serikali Kuu la muda mrefu kidogo, zaidi ya miaka minne, mitano, kuomba kupandishwa hadhi kwa Zahanati za Kata za Longuo, Ng’ambo na Msaranga, lakini bahati mbaya mpaka leo Serikali haijatujibu na tuna tatizo la huduma ya miundombinu ya afya katika Manispaa ya Moshi kwa sababu hatuna hospitali ya wilaya na hospitali ya wilaya Serikali haikuwa tayari kutukubalia ombi letu. Je, ni lini hadhi ya vituo hivyo itapandishwa ili tuwe na vituo vya afya vya kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Raphael Japhary Michael, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, uwepo wa zahanati umuhimu wake hauondoki kwa kuondoa zahanati kuifanya eti kituo cha afya, kwa hiyo msimamo wa Serikali kwanza ni suala la uwepo wa zahanati lakini pia na uwepo wa vituo vya afya. Pale ambapo inaonekana kwamba hakuna namna, baada ya kujiridhisha kwamba matakwa yote ya kutoka zahanati kwenda kituo cha afya, hapo ndipo Serikali tunafanya kupandisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sio rahisi kwa swali ambalo Mheshimiwa Mbunge ameuliza bila kujiridhisha kwamba yale matakwa ya kituo cha afya ambayo ni tofauti na zahanati yametimizwa. Inawezekana ndiyo maana na yeye mwenyewe anaridhika kwamba Serikali tunahakikisha tunajenga vituo vya afya tukizingatia ramani lakini pia na eneo ambalo zahanati zinatakiwa kuwepo na vituo vya afya vinatakiwa kuwepo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kituo cha Afya cha Hamai kilichopo Wilayani Chemba kina upungufu mkubwa wa vifaatiba. Kituo hicho ndicho kinachotumika kama hospitali ya wilaya, kinahudumia wananchi wote wa Jimbo la Chemba, lakini pili, majirani zetu kwa maana ya Chilonwa na Jimbo la Kiteto mpakani kule. Sasa nataka kujua Wizara imejipangaje kutupatia vifaatiba zikiwemo x-ray machines pamoja na ultrasound? La pili suala zima la ambulance yetu, imechoka haitamaniki, haithamaniki. Nataka kupata majibu ya Waziri kuhusiana na hicho kituo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu lililotangulia, kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vyote vya afya vinapelekewa vifaa. Niruhusu nichukue fursa hii kuiagiza MSD kuhakikisha kwamba zile oda zote ambazo zimepelekwa kuwe na msukumo wa kuhakikisha kwamba hivyo vifaa vinapatikana mapema ili viweze kutumika katika vituo vya afya kama Serikali tulivyokusudia. Pia ni ukweli usiopingika kwamba MSD safari hii wanakwenda kuagiza kutoka kwa manufacturer, sio habari ya kuagiza kutoka kwa mtu wa kati na kuna specifications ambazo lazima tuzingatie, lakini ni vizuri tukahakikisha jambo hili linafanyika mapema.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Kaka yangu Kandege, pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kuboresha hiki kituo muhimu cha Kiagata ambacho sasa kinatoa huduma kwa kiwango cha ufanisi, na pia kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kujenga vituo zaidi ya tisa katika Mkoa wa Mara, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuayavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa kituo cha Kiagata na hata hospitali ya Wilaya ya Butiama ina upungufu wa wataalam kwa kiwango cha asilimia 70, kwamba pia lipo tatizo kubwa la wataalam wa mionzi lakini vilevile hakuna x-ray kwa Wilaya nzima ya Bitiama ikiwemo hospitali ya Wilaya na hata kituo cha Kiagata.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inapeleka wataalam katika hospitali ya Butiama na Kituo cha Kiagata na hasa kipaumbele kikiwa ni wale watalam wa mionzi kwa ajili ya wakina Mama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Wilaya ya Butiama kwa mujibu wa sensa ina watu zaidi ya 200,003 na Butiama ni Wilaya ya kazi, watu wanakula wanashiba, population ya watu inaongezeka.

Vilevile kwa kuwa Wilaya ya Butiama ina kata 18 na ina vitongoji 370 lakini Kituo cha Afya ni kimoja tu cha Kiagata ambacho kinahudumia hata wananchi wote wa Wilaya y Butiama; Tarafa ya Makongoro iko mbali na Kiagata, Wananchi wa Makongoro wanapata shida sana kwenda Kituo cha Afya cha Kiagata;

(i) Ni mkakati gani sasa wa Serikali wa kuboresha Kituo cha Bisumwa ili kiwe sasa kituo cha afya, ili kisaidie Kata saba?

(ii) Serikali ina mkakati gani wa kuboreshga Zahanati ya Kirumi ili sasa isaidie Kata sita?

(iii) Na Serikali ina mkakati gani wa kuboresha Zahanati ya Buhemba ili iweze kusaidia wananchi wa Wilaya ya Butiama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Amina Makilagi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu nipokee pongezi ambazo ametoa kwa Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi inayofanya ya kupeleka huduma za afya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, anaongelea suala zima la uharaka wa kuhakikisha kwamba wanakuwepo wataalam, na hasa wataalam wa mionzi, ili kazi nzuri iliyofanyika Kituo cha Kiagata iweze kutoa matunda. Naomba nitumie fursa hii kumuagiza Mganga Mkuu wa Wilaya, miongoni mwa wataalam waliopo ateue angalau mtaalam mmoja akasomee kazi ya mionzi ili huduma ianze kutolewa ili huduma ianze kutolewa wakati Serikali inafikiria kupeleka wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametaja kituo cha afya lakini na zahanati kama tatu, sina uhakika kama ni swali moja lakini naomba itoshe tu nimambie Mheshimiwa Makilagi, kazi kubwa, nzuri ambayo anaipigania kuhakikisha hasa akina mama wanapata huduma ya afya, sisi kama Serikali tuko pamoja na yeye.

Naomba nitoe wito kwa halmashauri kuhakikisha kwamba maombi yote ambayo Mheshimiwa Amina Makilagi ameyatoa hapa yanazingatiwa katika bajeti hii ambayo inaandaliwa na sisi Serikali Kuu hakika hatutamuangusha. (Makofi)
MHE. PASCAL Y. HAO NG A: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa katika majibu ya Serikali ni kwamba zimetengwa milioni 37 zitakazotumika katika kuboresha wodi ya akina mama wanaojifungua; na kwa kuwa wodi hiyo ni wodi ambayo kwa kweli akina mama wanapata shida, wanalala akina mama wawili katika kitanda kimoja na kuna msongamano mkubwa sana;

Je, Serikali sasa inaweza ikatupa majibu rasmi wana Mbozi na wana Songwe kwamba hizo fedha ni lini sasa zitakwenda rasmi? Kwasababu tatizo hili si dogo, ni kubwa sana. Akina mama wanapata shida na wanaweza kupata magonjwa kwasababu kuna msongamano ambao kwa kweli si wa kawaida?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa pia katika Hospitali hii ya Wilaya ya Mbozi ambayo pia inatumika kama Hospitali Teule ya Mkoa wa Songwe kuna tatizo la ufinyu wa OPD; na OPD iliyopo pale ni ndogo sana na kuna msomngamano mkubwa sana.

Je, Serikali ipo tayari sasa kufanya upanuzi wa ile OPD ili iweze kuboreshwa na ichukue wagonjwa walio wengi zaidi kuliko hali iliyoko sasa ambayo wagonjwa ni wengi na OPD ni ndogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kujibu maswali yote mawili ya Mheshimiwa Haonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu ya msingi nimemwmbia Mheshimiwa Mbunge commitment ya Serikali kwamba katika bajeti ya mwaka 2020/2021 milioni 37 zimetengwa. Tafsiri yake ni nini? Ni kwamba hiyo inaonesha seriousness ya Serikali katika kuahidi na kuweka katika maandishi. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali, tukiahdi tunatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaongelea juu ya suala zima la ufinyu wa wodi, kwa maana kunakuwa na msongamano mkubwa wa wagonjwa katika ile hospitali ambayo inatumika kama ndiyo hospitali ya rufaa ya Mkoa. Ni ukweli usiopingika kwamba hospitali ile mwanzo haikuwa imekusudiwa kuwa hospitali ya Mkoa; lakini pia ni ukweli usiopingika Serikali imekuwa ikifanyakazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba huduma ya afya inasogezwa na ndiyo maana hata ukienda kwa Mheshimiwa Haonga unakuta kuna kituo cha afya cha Kisansa ambacho tukienda tukafanya shughuli nzuri na yeye ni shuhuda. Aendelee kuiamini Serikali, kwamba tutafanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba pale ambapo inahitajika tufanye upanuzi tutafanya pasi na kusita.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza:-

Kwa kuwa hospitali ya Wilaya Mpwapwa ilijengwa Mwaka 1975 na kwa kuwa wodi ya Wakina Mama wanaojifungua ni ndogo. Kama walivyosema wenzangu akina mama wanalala wawili, wanalala watatu ambapo ni hatari kaisa kuambukizana magonjwa.

Je, Mheshimiwa Waziri katika bajeti inayokuja, utatenga fedha kwa ajili ya kujenga jengo kubwa la wodi ya akina mama katika Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Seneta Lubeleje kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba hospitali za wilaya zilizojengwa miaka ya zamani ukilinganisha na uhalisia wa sasa hivi kumekuwa na upungufu wa baadhi ya majengo au msongamano umekuwepo kwasababu idadi ya watu inaongezeka. Naomba Mheshimiwa Mbunge akubaliane na kazi nzuri ambayo inafanya na Serikali. Tumeanza na hizo hospitali 67; kwa kadri Bajeti itakavyoruhusu na uhalisia na kwake pia tutatazama nini cha kufanya.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada za Serikali katika kujenga vituo vya afya na hospitali lakini vilevile vifaatiba pamoja na wataalam ni muhimu sana; na muhimu zaidi ni elimu kwa Watanzania namna ya kutumia hizi hospitali na vituo vya afya. Kwasababu tumeshuhudia sasa hivi wamezuka watu wanawadanyanya Wananchi wavue nguo zao za ndani wapungie juu wapate ujauzito, sijui wanawanyweshwa jiki na vitu kama hivyo vya aibu tena wanaofanyiwa aibu hizi ni akina mama.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa elimu kwa Watanzania ili wajue wkamba kuna mambo ambayo yanahitaji utaalam wa kidaktari na si uongo wa watu wanaojiita manabii na wachungaji wanaodhalilisha Watanzania katika mambo mbalimbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Joseph Raman Selasini, Mbunge wa Rombo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kujenga vituo vya afya na kupeleka huduma ya afya kama haitumiki hata umaana wenyewe unakua haupo. Naomba nikubaliane an Mheshimiwa Mbunge Selasini; lakini pia tukubaliane kwamba hii kazi si kazi ya Serikali peke yake. Sisi Waheshimiwa Wabunge tuna fursa katika forum mbalimbali ambazo tunakutana nazo, ni vizuri tukatoa elimu lakini pia hata maeneo ya makanisa, misikiti ni vizuri elimu ikapelekwa; si suala la kuiachia Serikali peke yake lakini pia Serikali haikwepi wajibu wa kuhakikisha wkamba elimu inapelekwa kwa wananchi.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuskhuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuulizwa swali la nyongeza.

Jimbo la geita Vijijini lina population ya watu takribani 450,000 mpaka 500,000 na halina Kituo cha afya hata kimoja. Je, Serikali haioni umhimu wa kutupatia kituo chaafya katika Kijiji cha Ibisabageni, Tarafa ya Isuramtundwe kwa ajili ya kuokoa wale akina mama wanaosafiri kwa umbali wa Kilometa 80 kuipata hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Musukuma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba uniruhusu kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Musukuma jinsi ambavyo amekuwa akipigania suala zima lafya na yeye amekuwa akijinasibu kwamba katika maeneo ambayo yamefanikiwa kujengwa hospitali nzuri ya Wilaya ni pamoja na kwenye Jimbo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, adhma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba inasogeza huduma za afya kwa wananchi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama ambavyo amekuwa akitoa imani kwa Serikali azidi kuiamini kwamba pale ambapo wananchi na hasa sehemu ambayo population ni kubwa kama ambavyo ametaja katika eneo lake hakika kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu kwa siku za usoni na wao tutawajengea kituo cha afya.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Awali ya yote naomba kwa niaba ya wananchi wa Madaba niishukuru sana Serikali pamoja na kutoa milioni 900 imetenga tayari milioni 500 kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Wilaya ya Madaba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile Halmashauri ya Madaba inachangamoto ya wauguzi kwa maana ya wataalam katika eneo la afya na kwa vile Mganga Mkuu sasa tangu amehama ni zaidi ya miezi 3 hatujapata Mganga Mkuu mwingine kwa ajili ya kutoa huduma. Na katika Kituo cha Afya cha Madaba ambacho kinatoa huduma tuna mganga mmoja tu ambaye yuko active. Ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba Madaba inapata Mganga Mkuu na inapata waganga kwa ajili ya kutoa huduma hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa vile katika zahanati hizi mbili ya Mbangamawe na Magingo wananchi wapo tayari kuendelea kutoa ushirikiano wa nguvu kazi na baadhi ya vitendea kazi. Ni lini sasa Serikali itatuhakikishia kwamba hizi fedha ambazo Serikali imekusudia kutupa zitapatikana ili wananchi waendelee kutoa nguvu kazi zao na kuhakikisha zahanati hizi zinakamilika na zinageuka kuwa vituo vya afya, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kipekee naomba nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mhagama pamoja na wananchi wa Jimbo lake na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla. Kama kuna sehemu ambayo wananchi wamekuwa wakijitoa katika kuhakikisha kwamba wanatoa nguvu yao ni pamoja na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza anaulizia suala la mganga ambaye alikuwa amepangiwa na nilikuwa nateta naye kabla sijaja kujibu swali hapa. Kuna mganga alikuwa amepangiwa sasa hivi yapata miezi miwili hajaenda kuripoti naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada tu ya kumaliza shughuli za Bunge leo nitafatilia nijue nini ambacho kimetokea ili nafasi ile kama mganga hajaenda kuripoti basi tumpeleke mganga mwingine kwa ajili ya kwenda kuziba pengo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ameongelea suala zima la upungufu wa watumishi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo kuna upungufu tunategemea kuajiri hivi karibuni na tutazingatia ikama ili maeneo ambayo yana upungufu mkubwa yaweze kupelekewa waganga.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anaongelea suala zima la wananchi kujitolea, jambo ambalo limekuwa likifanywa ndani ya Mkoa mzima wa Ruvuma na nini jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba pesa zinapelekwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge maeneo yote ambayo wananchi wanajitoa kama ilivyo katika Mkoa wa Ruvuma, Serikali itakuwa tayari fedha ikipatikana kuwaunga mkono wananchi.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Lupembe Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ina vituo vinne ambavyo vinafanya kazi lakini vichakavu. Pia wananchi kupitia mapato ya ndani na wananchi wenyewe tumejenga kituo cha afya cha Ikuna. Sasa katika hivi vituo vya zamani Kituo cha Kichiwa, Sovi, Matembwe na Lupembe ni lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya kukarabati na kuongeza majengo ili wananchi wa Lupembe waweze kupata huduma kama ilivyo maeneo mengine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kutoa majibu katika swali la msingi. Katika maeneo ambayo tumetenga fedha ili kuhakikisha kwamba huduma ya afya inaboreshwa ni pamoja na jimbo la Mheshimiwa Mbunge na atakumbuka kwamba katika vituo vya afya vya kuboreshwa ni pamoja na Kichiwa ambacho ametaja. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kadri fedha ya kwanza itakavyopatikana eneo la kwanza kupangiwa fedha itakuwa na kituo chake kwa sababu yeye amekuwa mstaarabu sana na amekuwa akifuatilia sana suala hili.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa mpango huu wa Serikali wa kupandisha hadhi Kituo cha Afya cha Moshi Arusha, lakini nilikuwa naomba Serikali, kwa sababu tunaelekea kwenye bajeti; na kwa sababu mchakato huo wa kupandisha hadhi kituo cha afya ni wa muda mrefu kidogo; ni lini sasa mpango huo utakamilika ili bajeti ya kukarabati hiyo miundombinu kwa ajili ya kuwa Hospitali ya Wilaya iweze kuingizwa katika bajeti ya mwaka huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, bado Moshi tuna tatizo kubwa la Vituo vya Afya. Tuna Vituo vya Afya viwili tu ambavyo vimeshazidiwa tayari; Kituo cha Afya cha Pasua na Kituo cha Afya cha Majengo. Nami naishukuru Serikali kwa kutupa shilingi milioni 400. Tumeleta maombi ya muda mrefu Serikalini ya kutusaidia kupandisha hadhi Vituo vya Afya vya Shirimatunda, Longuo B na Msaranga.

Je, ni lini Serikali itakubaliana na ombi letu? Kama hilo ombi haliwezekani, ni lini sasa itatujengea kituo kingine kimoja cha afya katika Manispaa ya Moshi?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii nimwombe Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu yeye ni sehemu ya Madiwani na katika mchakato wa kuhakikisha kwamba tunabadilisha hicho Kituo cha Afya ni pamoja na wao kutekeleza wajibu wao. Atusaidie kusukuma Halmashauri yake kufanya taratibu zile ambazo anatakiwa kuzifanya halafu sisi tuweze kumalizia.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameongelea juu ya suala zima la kubadilisha Zahanati kuwa Vituo vya Afya, ametaja nyingi lakini pia akawa na ombi kuwa, kama hilo haliwezekani ni vizuri basi tukafikiria suala la kujenga Kituo cha Afya kingine. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Zahanati zinaendelea kuwepo kama Zahanati kwa sababu Zahanati na Vituo vya Afya ni vitu viwili tofauti. Kwa hiyo, siyo azma ya Serikali kubadilisha Zahanati kuwa Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge, Zahanati zile zilizopo ziendelee kuwa Zahanati ila ombi la kuanzisha ujenzi wa Kituo cha Afya kipya, hilo tunaliweka katika matazamio ya siku za usoni.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa swali la msingi ni kuhusu Hospitali ya Mawenzi na Hospitali ya Mawenzi kusema ukweli imezidiwa sana; namna gani Serikali inaona umuhimu wa kuimarisha hivi Vituo vya Afya kama alivyouliza Mheshimiwa Japhary Michael na hasa Kituo cha Afya cha Kirua Vunjo Magharibi ambapo tangu kimefungulia wa Mheshimiwa Abdu Jumbe mwaka 1973 miundombinu yake ni chakavu sana na wala hakina hadhi ya kuwa Zahanati ili kiimarike kiweze kutoa huduma kama vituo vingine vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba vile Vituo vya Afya vilivyojengwa miaka ya zamani vilikidhi haja kwa kipindi hicho. Ukilinganisha na Vituo vya Afya ambavyo vimejengwa sasa, vile vingine vyote vya zamani vinaoneka vimechakaa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwanza tulianza kukarabati vile ambavyo vipo lakini pia tukaanza kujenga upya. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vituo vyote vya afya vinakuwa na hadhi ya Vituo vya Afya ili viweze kutoa upasuaji wa dharura kwa mama mjamzito.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbatia, kama ambavyo Serikali imekuwa ikipitia kuona takwimu Vituo vya Afya vipi vichakavu na cha kwake tutakipitia.
MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa ruhusa yako naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais, Jemedari Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa juhudi zake na msimamo wake wa kuhakikisha Watanzania tunapata huduma za afya. Ukiangalia kwenye Mkoa wetu wa Pwani, Vituo vingi vya Afya, Zahanati na Hospitali za Mkoa zimepata vifaa tiba na wataalam mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza: Kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameonyesha njia ya kutaka Watanzania wapate huduma bora na sahihi kwa wananchi wake: Je, hawaoni kwamba kwa kuwafanya Waganga Wafawidhi na wa Vituo vya Afya au Zahanati kusimamia masuala ya Uhasibu ni kuipelekea kada hiyo kuacha kazi zake za kutibu na kuhangaika maeneo mbalimbali kwenda kununua dawa, kwenda kufuata vifaa tiba na kuacha kutibu wagonjwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Kwa kuwa Serikali imeonyesha nia ya kuomba kibali kwa ajili ya Wahasibu na mpaka leo hii hicho kibali hakijapatikana; kwa nini msichukue wataalam wa uhasibu ambao wamemaliza masomo yao, wako maeneo mbalimbali Tanzania na wakafanya kazi hizo kwa kujitolea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, niruhusu kwa niaba ya Serikali nipokee pongezi ambazo Mheshimiwa Mbunge ametoa. Naye amekuwa ni miongoni mwa champions ambao wamekuwa wakipigiania suala zima la afya, naye anastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika swali lake anaongelea suala zima la kwamba Waganga wanaacha kazi zao za kitaaluma na wanaanza kufanya kazi ya fedha; katika majibu yangu ya msingi nimemwambia kwamba tumeajiri watumishi wa Kada ya Uhasibu 335.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba kwa muda mfupi ambao tumewapa hiyo taaluma ni ili wawe na uelewa wa jumla, lakini Uhasibu ni professional ambayo haiwezi ikasomewa ndani ya muda mfupi huo. Kwa hiyo, hawaachi kazi yao ambayo wameajiriwa nayo kuanza kufanya kazi ya usimamizi wa fedha, lakini ni vizuri at least wakajua nini ambacho kinaendelea kulikoni kutojua kabisa. Huo ndiyo msingi wa elimu ambayo imetolewa kwa hao Waganga.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anasema kwamba ni vizuri, pamoja na kwamba tumeomba kibali cha kuajiri, sasa kuna wengine ambao wamemaliza taaluma ya Uhasibu wako Mtaani tuwaajiri wajitolee. Sina uhakika sana na kwa sera yetu haijatokea mahali hata pamoja ambapo tunataka mtu afanye kazi asilipwe.

Mheshimiwa Spika, tuendelee kuwa na subira, Serikali ni sikivu na jana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya utawala alisema tunaenda kuajiri watumishi mbalimbali 45,000. Ni imani yangu kubwa katika hao watakaoajiriwa ni pamoja na Wahasibu wakaokwenda kufanya kazi hizo.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili madogo ya nyongeza; na unipe ruhusa niwape pole wananchi wa Monduli, hasa wa Mto wa Mbu ambao wamekubwa na mafuriko kwa muda wa wiki moja sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, Serikali imesema imetenga shilingi bilioni saba kwa ajili ya ujenzi wa kilometa tisa; lakini bilioni saba hizo inawezekana zisipatikane kwa wakati. Nataka kujua commitment ya Serikali ya kuhakikisha kwamba walao barabara hii inawekwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Barabara hii ya Monduli Juu ambayo Waziri anasema ipo katika hali ya upembuzi yakinifu, upembuzi yakinifu umekamilika na document zote zipo tayari. Je, ni lini hasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Julius Kalanga yenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji Mdogo wa Mto wa Mbu unaufahamu vizuri. Na Mheshimiwa Mbunge amekuwa akipigania kwa sababu adha ambayo imekuwa ikipatikana kila wakati mvua zinaponyesha mafuriko yanakuwepo eneo lile. Kwanza kipekee naomba nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akilipigania eneo hili kwa muda mrefu. Naomba nimhakikishie, katika bajeti ya mwaka 2020/2021 tutaanza na mifereji na ujenzi wa kilometa moja utaanza ili tupunguze adha kwa wananchi wa Mto wa Mbu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ameongelea barabara ya kwenda kwa Marehemu Sokoine. Kama anavyokiri hata yeye mwenyewe, kwamba usanifu ulishakamilika. Naomba nimhakikishie, kufanyika kwa usanifu tafsiri yake ni kwamba, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi kwamba fedha ikipatikana nako ujenzi utaanza. Aendelee kuiamini Serikali kama ambavyo tukiahidi daima tumekuwa tukitekeleza.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza; lakini uniruhusu niseme jambo moja dogo ambalo siku zote nimekuwa nikitafakari wahenga wakisema kua uyaone, lakini hatimaye nimeyaona jana goli kuwa kona kwa watani zangu wa Yanga; kwa kweli, nimestaajabu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba swali langu dogo la nyongeza lipate majibu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Serikali imedhamiria kuhakikisha barabara zote ambazo ziko kwenye ahadi zinajengwa na kukamilika kwa kiwango cha lami ikiwemo Barabara ya kutoka Buhongwa – Lwanima – Kishiri mpaka Igoma. Sasa, ni lini Serikali itakuwa tayari kuhakikisha barabara hii inakamilika kwa kiwango cha lami kama ambavyo iliahidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambayo Mheshimiwa Mbunge anaitaja ni barabara ambayo iko chini ya TARURA. Na kipekee Mheshimiwa Mbunge amekuwa akiipigania barabara hii kwa muda mrefu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge; usanifu wa barabara hii umeshakamilika; na kitakachofuata katika bajeti ya mwaka 2020/2021 tutaanza kuijenga hatua kwa hatua, ili barabara yote iweze kukamilika.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji Mdogo huu wa Mto wa Mbu ni sawasawa na Mji Mdogo wa Karatu; kwa maana ni miji ambayo watalii wanapita kuingia katika Hifadhi ya Manyara na Hifadhi ya Ngorongoro.

Je, Serikali sasa haioni kuna umuhimu wa kuwa na mpango mkakati wa kuendeleza miji hii kwa sababu ni kitovu cha kuingia katika Hifadhi zetu za Taifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Mbunge ameongelea Mji Mdogo wa Mto wa Mbu na Mji wa Karatu; ni kweli ni miji ambayo ni ya pekee kwa sababu ni lango katika watalii wanapoenda kutembelea mbuga zetu. Kama ambavyo Serikali imekuwa na mpango kupitia TSSP tumekuwa tukiendeleza miji kwa kujenga barabara za kiwango ambacho ni kiwango kizuri. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuridhika na Serikali yetu hatua kwa hatua tunamaliza hiyo miji ambayo tulianzanayo nina hakika, katika mji ambao ameutaja kwa sababu ni jicho la kipekee kwa watalii nao hakika hatutauacha.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kumuuliza Naibu Waziri, kwa nini Nyanghwale haitengewi pesa za maendeleo ya barabara ilhali kuna barabara ambazo zimeharibika vibaya yakiwemo madaraja kutoka Nyanghwale pale makao makuu kwenda Lushimba. Ni kwa nini Serikali haitutengei fedha za maendeleo ya barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Amar, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ya CCM ambayo na yeye Mheshimiwa Mbunge anatokana na CCM anajua kabisa kumekuwa hakuna upendeleo katika kupeleka maendeleo katika nchi yote kwa ujumla. Kwa kuwa yeye ni sehemu ya Madiwani ni vizuri basi wakahakikisha kwanza wanaanza kutenga wao na sisi Serikali Kuu tukapata taarifa. Kimsingi hakuna hata eneo moja ambalo hatutengi fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa jengo la ICU muhimu sana na kwa kuwa mradi ule mpaka sasa hauna fedha na Serikali imesema itatenga fedha mwaka huu wa fedha, je, Serikali iko tayari kupeleka angalau hizo milioni 200 za dharura?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa idadi ya watumishi ni ndogo sana hususan kitengo cha nursing, je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kuongeza angalau watumishi sita katika Hospitali ya Wilaya?

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na maswali hayo, nipongeze sana majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwanne Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Tabora, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Serikali, naomba tupokee pongezi ambazo Mheshimiwa amezitoa. Kipekee naomba na mimi nimpongeze kwa jinsi ambavyo amekuwa akipigania kuhakikisha afya na hasa ya akina mama inaboreshwa katika Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza anaomba walau Serikali itoe jumla ya shilingi milioni 200 za dharura. Hata hivyo, katika majibu ya msingi na swali la msingi kinachoombwa ili kumalizia majengo yote mawili ni jumla ya shilingi milioni 200. Naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuiamini Serikali, tumeahidi kwamba katika bajeti ya 2020/2021 tunaenda kutekeleza na hii inatokana na baadhi ya maboresho makubwa ambayo yamefanyika katika Hospitali ya Urambo ambapo sasa hivi hata makusanyo yanayokusanywa pale ni mengi. Naomba Mheshimiwa aendelee kuiamini Serikali, tutatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili anaomba kuongeza idadi ya watumishi walau sita. Juzi Waziri mwenye dhamana amejibu akieleza namna ambavyo Serikali inaenda kutoa jira zisizopungua 45,000. Katika watumishi watakaoajiriwa upande wa afya, hakika nimhakikishie Mbunge na Tabora kwa ujumla wake hatutaisahau. (Makofi)
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii uliyonipa ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tabu wanayopata wananchi wa Urambo, wanapata wananchi wangu wa Wilaya ya Mpwapwa, Jimbo la Kibakwe, Kata ya Mlunduzi ambayo ina zahanati tatu na zahanati hizi majengo yameshakamilika lakini milango, madirisha, ceiling board havijawekwa, kwa hiyo wanawake na watoto wanapata shida wakitafuta matibabu mbali na maeneo yao wakati majengo yako pale. Je, ni lini Serikali itakamilisha majengo yale ya zahanati ya Kata ya Mlunduzi, Jimbo la Kibwakwe ili wananchi wa pale waweze kupata huduma ya karibu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Felister Bura, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hicho anachosema Mheshimiwa Mbunge ndiyo uhalisia maana yeye mwenyewe anakiri kwamba almost ni kama majengo yamekamilika imebaki vitu vichache tu ili kukamilisha majengo hayo. Naomba nichukue fursa hii kumuagiza Mkurugenzi Mtendaji ahakikishe kwamba tathmini inafanyika kwa sababu katika hayo ambayo anayasema ni pesa kiasi kidogo sana kinahitajika ili kuweza kukamilisha zahanati hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimtoe wasiwasi. Kama kuna mikoa yenye neema kwa sasa hivi ambayo watumishi wengi wa Serikali wanapenda kuhamia ni pamoja na Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo, adha ya ukosefu wa watumishi kwa Dodoma itabaki ni historia.
MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana na ninakupongeza kwa kutupatia tablet hizi. (Makofi)

Pili, hili swali niliuliza mwaka 2016, lakini naishukuru Serikali leo wamejibu kwa vitendo. Kweli Kituo cha Afya Masoko sasa hivi utasema upo Ulaya, nashukuru sana. Pamoja na shukrani hizo; je, ni lini Serikali itatimiza au itakamilisha wafanyakazi 22 waliobakia ili kituo kiendane sawasawa na kilivyo? Swali la kwanza hilo.

Swali la pili; kwa kuwa hakuna gari maalum ya wagonjwa hiyo unayosema, lakini kwa kuwa umenipa matumaini kwamba mtatafuta gari nyingine: Je, lini hiyo gari ya Kituo cha Afya cha Kilwa Masoko itapatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, niruhusu nipokee pongezi za Mheshimiwa Bungara, maana huwa zinatolewa mara chache sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anauliza ni lini upungufu wa watumishi 22 utatatuliwa ili hadhi ya Kituo cha Afya ambacho anasema ni sawa na kuwa Ulaya kitaweza kutoa huduma kukiwa na ikama ambayo inatakiwa?

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ameendelea kuiamini Serikali ya CCM ikiahidi inatekeleza na utekelezaji ni pamoja na swali ambalo aliliuliza, nami nampongeza kwa kuuliza swali na Serikali tumemjibu kwa vitendo. Naomba nimhakikishie ni azma ya Serikali kuhakikisha maeneo yote ambayo Vituo vya Afya vimefunguliwa tunapeleka watumishi kwa kadri nafasi za ajira zinavyopatikana na Kilwa hatutasahau.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anaulizia suala la kuwepo gari. Gari lililopo aina ya Maruti linafanya kazi, lakini kama tulivyokiri katika majibu yetu kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunapata gari zuri zaidi kwa kushirikiana Halmashauri yake, ni vizuri nao katika bajeti; maana kama kuna Halmashauri ambayo inafanya vizuri katika makusanyo ni pamoja na Halmashauri yake maana zao la ufuta linaingiza fedha nyingi. Ni vizuri nao Halmashauri wakatenga na sisi Serikali tukashirikiana ili gari ziweze kupatikana kwa ajili ya wananchi.
MHE. RAPHAEL H. MICHAEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri ya Kikanuni, lakini kutokana na jiografia ya Manispaa ya Moshi, Kata ya Msaranga, Ng’ambo na Kibororoni zipo karibu na wananchi hawa wanashirikiana pamoja katika kutafuta huduma za afya. Sasa je, Serikali kwa maelekezo hayo kwamba wanahamasisha kujenga vituo vya afya, ni lini itatupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya katika Kata hiyo ya Msaranga ili tuweze kusaidia hizo Kata tatu kwa pamoja ili wananchi wapate huduma za afya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Manispaa ya Moshi tuna ombi la muda mrefu kwa Serikali kuhusiana na Hospitali ya Wilaya na kuna uhitaji mkubwa sana ili kusaidia wagonjwa ambao wamezidi Hospitali ya KCMC na Hospitali ya Mawenzi. Je, ni lini sasa ombi letu litakubaliwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anaongelea Kata mbili ambazo ziko tayari kushirikiana ili waweze kupata Kituo cha Afya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Serikali tuko tayari pale ambapo wazo limeanzia kwa wananchi na eneo linakuwepo na utayari wa wananchi katika kujenga Kituo cha Afya, nasi kama Serikali tunapeleka nguvu yetu.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anaongelea juu ya suala zima la ujenzi wa Hospitali ya Wilaya kwa ajili ya Manispaa ya Moshi. Katika jibu langu la msingi nimemwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba huduma kwa ajili ya sehemu ambazo hakuna Hospitali ya Wilaya zinapatikana na ndiyo maana sisi kama Serikali kwa kushirikiana na St. Joseph tumewapa hadhi ya kuwa kama Hospitali ya Wilaya kwa ajili ya kutoa huduma hiyo, lakini itekelezwe kwa muda wa mpito pale ambapo Hospitali ya Wilaya haipo.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Serikali tuko tayari kama ambavyo tumeanza maeneo mengine, tutahakikisha kwamba hata Manispaa ya Moshi nayo inapata Hospitali ya Wilaya.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Vilevile napenda kutoa shukrani kwa Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya msingi niliyosema shule hii ni shule pekee katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, shule pekee yenye inawachukuwa watu wenye mahitaji maalum, kwa takwimu hiyo utaona kabisa kwamba bado kuna tatizo la miundombinu, shule hii inahitaji mabweni na ndiyo maana inakuwa na takwimu ndogo ya walemavu kwa sababu walemavu wengi kutoka vijijini wanashindwa kumudu kuandikishwa kwenye shule hii kwa sababu ya ukosefu wa mabweni, lakini siyo hivyo hata wale walimu hao anaowataja...

MWENYEKITI: Uliza swali basi Mheshimiwa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja; je, Mheshimiwa Waziri haoni umuhimu wa kujenga mabweni kwenye shule hii ili watoto wanaotoka nje ya Halmashauri hii waweze kumudu kuingia shuleni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa sababu ya mahitaji ya wanafunzi hawa wanatakiwa wafuatiliwe kule wanapokaa manyumbani kwa sababu hawakai bweni kwahiyo panahitajika usafiri wa walimu hao kuwafuatilia kule wanapoishi kuona maendeleo yao namna gani wanavyo catch yale masomo. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwanunulia vifaa kama vile mapikipiki hawa walimu watatu waliobaki ili waweze kumudu kuwafuatilia hawa watoto manjumbani kwao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tunakubaliana na Mheshimiwa Mbunge, kwanza tunaunga jitihada za Mheshimiwa Mbunge katika kuhakikisha kwamba hawa wanafunzi wenye uhitaji maalum wanapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge jana nilipata fursa ya kuongea na mkurugenzi na tukakubaliana kwamba hicho kiasi cha shilingi milioni 50 itatengwa kuanzia mwezi Desemba wakati tutakapokuwa wanafanya review ya bajeti yao kwa sababu na wanaona ni jambo la muhimu sana kuhakikisha watoto hawa wanakuwa katika mazingira yaliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika swali lake la pili anaongelea swala zima la usafiri ili walimu waweze kwenda kupata fursa kwenda kuwabaini hata wanafunzi wengine ambao wanashindwa kujiunga kutokana na adha iliyoko huko, naomba ni muhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni azma ya Serikali, siyo walimu peke yao ni pamoja watumishi wote ikiwepo wale wa Ustawi wa Jamii kuhakikisha kwamba tunawabaini watoto wetu wote bila kujali hali zao ili waweze kupelekwa katika maeneo ya kuweza kujufunza sawa na watoto wengine ambao hawana ulemavu.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, pale jimboni Kondoa tunazo shule mbili, Shule ya Iboni na Shule ya Ubembeni ambazo zinavitengo vya watoto wenye mahitaji maalum zote ziko kata moja ya Chemchem ambayo ni kata ya katikati kabisa katika jimbo zima. Hali ya mapato yetu ya ndani ya Halmashauri ni ndogo sana ambayo imetupelekea mpaka mimi mfuko wa jimbo kuweza kusaidia miundombinu stahiki kwa ajili ya wale watoto pamoja na choo, walimu pia hatuna.

Je, Waziri ni lini unaweza ukafanya utaratibu wa kutuupa uzito na kuja kufanya tathimini ya kina ili tuweze kuweka miundombinu stahiki na walimu wa kututosheleza ukizingatia watoto hao wenye mahitaji maalum wanaendelea kuongezeka siku hadi siku?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Sannda kwa jitihada zake kwa kutumia mfuko wa Jimbo ili kuhakikisha kwamba miundombinu wezeshwi inajengwa katika shule hizo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba watoto wote wenye uhitaji maalum hawaachwi nyuma na suala zima la uhitaji wa walimu ambao wanatakiwa waajiriwe naomba nimuhakikishie kama sisi Serikali tutazingatia maombi yake.
MHE. JOYCE J. MUKYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, Shule ya Msingi ya Uhuru iliyoko Arusha ni shule pia yenye watoto walemavu, shule hii inashida pia ya miundombinu, vyoo vyake havifai ukizingatia kuwa walemavu wengi au baadhi ya walemavu ni wale ambao wanatambaa, ukiangalia vile vyoo ni vichafu, havifanyi kazi vizuri maji mpaka yanatitirika nje na tunavyoelewa ukiongelea swala zima la vyoo ni afya.

Je, Serikali itarekebisha lini miundombinu ile ya vyoo katika hile shule ya Uhuru ya Arusha Mjini ili kuwasaidia walemavua hawa watoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba nichukuwe fursa hii kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Arusha kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika swali langu la msingi nikimuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri


ya Liwale naomba nitumie fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Jiji Arusha kwa sababu nina uhakika wanavyanzo vya mapato vya kutosha, atizame namna gani wataweza kuboresha miundombinu ili wanafunzi wetu wenye uhitaji maalum wasome katika mazingira yaliyo bora.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu haya ingawa wamekosea sana majina ya vijiji vyangu na kata zangu na pale napenda kutoa marekebisho kwamba pale Taweta ni Kijiji cha Tanganyika siyo Tanga, sisi kwetu hatuna Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada za Serikali lakini jimbo la Mrimba lina changamoto kubwa sana ukizingatia sisi ni wakulima kama asilimia 99 kwa hiyo madaraja haya yasipojengwa kwa wakati kwa hiyo mazao mengi yanashindwa kufika sokoni na wakulima kuwa maskini miaka yote.

Je, pamoja na bajeti hii imetengwa, Serikali haioni kwamba iliangalie Jimbo la Mlimba kwa akina ya pekee kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanapata miundombinu hii ukizingatia mito mingi mikubwa kwa mfano hii Tanganyika kuna huo Mto Kilombero ndiyo unapita huko, chini kuna mamba wengi lini mtafanya na kunatakiwa daraja kubwa.

Je, Waziri mara nyingi naongea na wewe upo tayari sasa kutembelea hilo Jimbo la Mlimba hivi uone hali halisi na uone kwamba kunajitihada za kujenga haya madaraja uone wananchi wanavyoteseka na mara nyingi nakuomba lakini hutaki kwenda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza atuwie radhi kwa kukosea majina ya vijiji vyake hatukukusudia hilo, lakini na yeye mwenyewe amekiri kwamba tumetenga kiasi cha shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuanza kujenga hilo daraja ambalo ni kubwa lakini kiasi cha shilingi 127; naomba Mheshimiwa Mbunge aridhike na jitihada ambazo zinafanywa na Serikali kwamba ni azma yetu kuhakikisha kwamba wananchi wa Mlimba wanapata madaraja na barabara za uhakika katika kipindi chote na mimi nashukuru, leo ameongea hajalia na sisi tunamhakikishia haitatokea kulia tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Susan amesema amekuwa akiniomba twende Mlimba naomba nimhakikishie nipo tayara ilikuwa ni swala tu la muda tupange na yeye mwenyewe tumewasiliana kunapindi fulani akasema kipindi hiki mvua zinanyesha sana hatuwezi kwenda, niko tayari.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la makorongo na mahitaji ya madaraja katika majibo ya vijijini imekuwa kubwa sana na kwa kuwa maeneo haya yanatatiza na kuzuia huduma za jamii nyakati za masika, katika Jimbo la Mbulu Mji kuna Daraja la Gunyoda linalounganisha Halmashauri ya Mbulu Mjini na Halmashauri ya Mbulu Vijijini; mahitaji ya ujenzi wa daraja lile ni zaidi shilingi milioni 600 na kwakuwa fedha tunazopata kutoka TARURA kwenye jimbo la Mbulu Mji ni shilingi milioni 600 na hazitaweza kusaidia ujenzi wa daraja hilo pamoja na maeneo mengine nchini. Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka mpango mkakati kwa kuainisha baadhi ya maeneo hayo ili tuweze kutatua tatizo hili linalokwaza jamii katika kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema katika swali lake kuna maeneo ambayo yanauhitaji maalum na kiasi cha fedha ambacho kinatakiwa kitumike kingi na yeye mwenyewe katika swali lake anasema kiasi ambacho TARURA Wilayani kwake wanapangiwa kiasi kidogo, ni vizuri tuendelee kushirikiana tuone maeneo hayo ili tuwe na mpango mahususi katika kuhakikisha sehemu ambazo inahitajika fedha nyingi ili kuwe na andiko maalumu kwa ajili ya kutatua maeneo yenye matatizo makubwa kama hayo.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipatia nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa matatizo yaliyopo Jimbo la Mlimba yanafanana na matatizo yaliyoko katika Jimbo la Kavuu na kwa kuwa nilikwisha omba maombi maalumu kwa ajili ya matengenezo ya daraja linalounganisha Kata ya Chamalemu D na Mwamwamapuli. Je, Serikali sasa ina mpango gani wa kupeleka pesa kwa ajili ya kutengeneza daraja hilo hili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma za afya katika Kata ya Kibaoni badala ya kuzunguka Kata ya Mbede?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaondolea adha wananchi ili wasilazimike kuzunguka umbali mrefu wakati ingewezekana kujenga daraja ili wananchi wasitembee umbali mrefu. Naomba nimhaikikishie Mheshimiwa Mbunge ni vizuri baada ya Bunge hili, baada ya kipindi hiki tuwasiliane na coordinator wa Mkoa tujue uwalisia na uhitaji kwa ajili ya daraja hilo ambalo linaweza likajenga ili wananchi wasilazimike kutembea umbali mrefu wakiwa wanafuata huduma ya afya ambayo na yeye mwenyewe anaridhika jinsi ambavyo huduma hii inatolewa kwa karibu, lakini adha imekuwa ni hilo daraja.
MHE. JOEL M. MWAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, majibu yanayotia moyo kwa wananchi wa Jimbo la Chilonwa. Pia nishukuru kwa ujumla wake jibu limekuwa la jumla mno kwa halmashauri lakini kwa jumla mno kwa Jimbo la Chilonwa, kwamba barabara nyingi zimetengezwa mwaka jana na nyingi zimepangwa kutengezwa mwaka huu. Sasa ombi langu kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa mwaka huu wa fedha 2019/2020 ambapo zimetengwa bilioni 1.366, naiomba Serikali ifanye kila linalowezekana kuhahikisha kwamba barabara hii ya kutoka bwawani kuja Ikowa angalau inatengenezwa na angalau iwe inatengenezwa kwa zile sehemu korofi ili iweze kupitika kipindi kizima cha mwaka. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS,TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Makanyaga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu ya msingi kwamba uhitaji kwa ajili ya kukamilisha barabara hii ni shilingi milioni 668.2, ni kiasi kingi cha fedha na katika bajeti ambayo wametengewa ni bilioni 1.366 maana yake ukisema unamega kiasi chote barabara zingine ambazo nazo zina uhitaji maalum zitakosa kutengenezwa. Naomba Mheshimiwa Mbunge avute subra kama ambayo nimejibu kwamba Serikali inajitahidi kutafuta kiasi kingine cha fedha ili tuweze kutengeneza barabara hiyo iweze kupitika katika vipindi vyote. Katika mikoa ambayo sisi kama Taifa kipaumbele kwa barabara ni pamoja na Dodoma, ndio maana hata bajeti yake imetengwa nyingi ukilinganisha na mikoa mingine.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais alipokuja Geita aliweza kunipatia Hospitali ya Wilaya itakayojengwa Kata ya Buseresere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, naomba niulize swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, naipongeza Serikali kwamba imekusudia kuajiri watumishi 550 lakini kwa kuwa Halmashauri ya Geita tuna upungufu mkubwa sana tungependa kujua ni lini sasa hao watumishi wataletwa ili waweze kuanza kufanya kazi katika Halmashauri ya Geita? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa katika Jimbo la Busanda kuna vituo vya kutolea huduma viwili ambavyo vimekamilika kabisa, vinatakiwa tu kufunguliwa, Buziba pamoja na Magenge. Napenda kupata kauli ya Serikali ni lini sasa watahakikisha vituo hivi vimefunguliwa kwa sababu vimekamilika kabisa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Lolesia Bukwimba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Serikali, naomba nipokee pongezi ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitoa kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza anauliza ni lini watumishi watapelekwa ili kuweza kuziba pengo la upungufu huo mkubwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mchakato uko kwenye hatua za mwisho kabisa kwa sababu katika suala la kuajiri lazima taratibu zote zifuatwe. Namwondoa mashaka muda si mrefu watumishi wataweza kupelekwa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili anaongelea vituo vyake vya afya viwili ambavyo tayari vimeshakamilika, anachotaka kujua ni lini vituo hivyo vitafunguliwa. Kama azma ya Serikali ilivyo kwamba vituo vile vya afya vinajengwa ili vianze kutoa huduma, sina uhakika kama tayari kama vifaa vyote vilishapelekwa. Kama vifaa vilishapelekwa ni jambo jema kinachotakiwa ni kupeleka watumishi ili vituo hivyo vifunguliwe vianze kutoa huduma. Ndiyo makusudi ya Serikali na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na matatizo makubwa ya kijiografia yaliyoko katika Visiwa vya Ukerewe yanayoathiri utoaji wa huduma za afya lakini tuna madaktari 3 pekee kati ya 10 wanaotakiwa, tuna waganga wasaidizi 5 pekee kati ya 43 wanaotakiwa na tuna wauguzi 80 pekee kati ya 289 wanaotakiwa. Nini kauli ya Serikali wanayoweza kuwaambia wananchi wa Ukerewe juu ya kuboresha huduma za afya kwa kutoa wahudumu wa afya kiasi kinachotakiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo yana upungufu mkubwa wa watumishi, wakati tunaajiri hao 550 tutazingatia. Naamini na Ukerewe nao hatutawasahau, ipo nia kubwa kuhakikisha kwamba tunapunguza hilo pengo la upungufu wa watumishi. Naomba nimhakikishie Mbunge tutazingatia katika mgao.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki Serikali imefanya jitihada kubwa sana za kujenga hospitali, vituo vya afya, zahanati na kadhalika. Kwa hili kama Kambi Rasmi ya Upinzani tulivyosema jambo zuri lazima tulipongeze, kwa hiyo, napongeza sana jitihada hizi ambazo zimefanyika katika kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tumetatua tatizo moja tumekaribisha tatizo lingine. Watumishi katika sekta hii ya afya ni wachache sana. Katika jimbo langu kwa mfano kuna upungufu wa asilimia 52 ya madaktari na wahudumu wengine katika sekta mbalimbali za afya. Nataka Serikali itueleze mkakati ambao utakwenda sambamba na ongezeko hili la hospitali na vituo vya afya ili sasa wananchi wapate ile huduma ambayo Serikali imekusudia waipate na ambayo ni haki yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee naomba kupokea pongezi kutoka kwa Kambi Rasmi, ni jambo ambalo limekuwa likifanyika mara chache sana. Sasa ikitokea ni wajibu na sisi tu-recognize hiki ambacho kimefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba huduma za afya zinasogezwa jirani na wananchi. Ni ukweli usiopingika kwamba sasa hivi wananchi wengi wanavutiwa kwenda kupata huduma kwenye vituo vyetu vya Serikali tofauti na vile vya mashirika ya watu binafsi na dini. Naomba nimhikishie Mheshimiwa Mbunge hao watumishi 550 ambao tutakuwa tumewaajiri na kuwasambaza hivi karibuni ni mchakato wa kuendelea kuajiri na wengine kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu ili tupunguze adha ya mwananchi kupata huduma kwa urahisi ikiwepo ni pamoja na Rombo ambayo wana Mbunge ambaye ni makini ameweza ku-recognize kazi nzuri inayofanywa na Rais wetu.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeifanya katika Mkoa wa Rukwa kutujengea Hospitali za Wilaya. Wakati nauliza swali hili tulikuwa hatujajengewa hospitali hata moja lakini ndani ya kipindi kifupi hospitali na vituo vya afya zimejengwa. Kwa hiyo, naipongeza Wizara na Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, hakika kazi ameifanya, Mwenyezi Mungu ambariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, sasa naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni lini sasa hospitali hizi zitaanza kufanya kazi na kuletewa vifaa tiba ikiwemo X-ray, MRI na vifaa tiba vingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali sasa ina mpango gani wa kutuletea madaktari bingwa, manesi na wafanyakazi wa kada nyingine zote katika hospitali hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Serikali tunazipokea pongezi ambazo zinatoka kwa Mbunge na naamini na Wabunge wote wanatoa pongezi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza anataka kujua ni lini sasa hospitali hizo ambazo zimejengwa zitafunguliwa ili zianze kutoa huduma kama zilivyokusudiwa. Naomba nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine, ni azma ya Serikali na ndiyo maana tulianza na majengo 7 yakamilike na yakishakamilika yaanze kutoa huduma wakati tunaongezea fedha zingine kwa sababu ili hospitali za wilaya zikamilike yanahitajika majengo yasiyopungua 22. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pale ambapo majengo yakishakuwa tayari, vifaa vikipelekwa tutapeleka watumishi ili wananchi wapunguziwe adha ya kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kufata huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ujenzi, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba wanakuwepo watumishi wa kutosha. Ndiyo maana tunaenda kuajiri hao 550, ni njia ya kuanza kupeleka wengine sio kwamba 550 ndiyo mwisho, hapana, tutaajiri na wengine kwa kadri bajeti itakavyoruhusu. (Makofi)
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Sisi kwetu pale Kondoa hospitali tunayo lakini hospitali ile inahudumia zaidi ya Halmashauri tatu za Chemba, Kondoa Vijijini, Babati na wakati mwingine mpaka Hanang. Kwa hiyo, mahitaji ya huduma yamekuwa ni makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunaipongeza Serikali kwa kukamilisha ile barabara ya kutoka Dodoma - Babati. Kunapokuwa na maendeleo na changamoto zinaongezeka sana. Kukamilika kwa barabara ile kumeongeza sana mahitaji ya huduma ya hospitali ikiwemo huduma za dharura. Nimelia sana kuhusiana na suala la ambulance, tuna tatizo kubwa sana la ambulance. Ni lini sasa Serikali itaipatia Hospitali ya Mji wa Kondoa ambulance mpya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Edwin Sannda, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kwa niaba ya Serikali kupokea pongezi ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Mbunge. Mheshimiwa Mbunge wakati anajenga hoja yake anaeleza jinsi ambavyo wananchi wengi wanalazimika kwenda kutibiwa kwenye Hospitali ya Kondoa Mji na hii tafsiri yake ni kwamba huduma inayotolewa pale ni nzuri ndiyo maana wananchi wanalazimika kutoka hata Chemba kwenda kupata huduma pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Serikali kuhakikisha kwamba inapunguza adha kwa wananchi kutembea umbali mrefu ndiyo maana hata Halmashauri ya Chemba inajengewa Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, hiyo influx ambayo imekuwepo itapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la msingi ambalo anataka kujua lini Serikali itapeleka ambulance ili kupunguza adha, amesema mara nyingi sana na Serikali ni sikivu, katika mgao ambao utapatikana kwa siku za usoni hakika Kondoa hatutaisahau.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Nkasi ni miongoni mwa Wilaya ambazo ziko Mkoa wa Rukwa na mpakani, zinapakana na nchi ya Kongo na Burundi na kumekuwa na mlipuko wa magonjwa ikiwepo ugonjwa wa Ebola. Nataka kujua mkakati wa Serikali, haioni ni muhimu sasa kuipa Wilaya ya Nkasi kipaumbele cha kujenga Hospitali ya Wilaya ili kuepukana na matatizo ambayo yanaendelea kujitokeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu ya msingi ni kwamba kwenye orodha ya Hospitali za Wilaya zinazojengwa ndani ya Mkoa wa Rukwa na Nkasi nimeitaja. Inawezekana Mheshimiwa Mbunge alikuwa haijaingia lakini kama hiyo haitoshi hivi karibuni katika mgao wa gari kwa ajili ya chanjo na ameongelea suala la Ebola na Nkasi nayo ipo katika mgao. Kwa hiyo, ni namna ambavyo Serikali imekuwa ikitilia maanani mahitaji na imekuwa ikitekeleza.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme sikuwa na hakika kwamba, swali hili lilikwenda TAMISEMI na binafsi swali hili tulilielekeza Wizara ya Ardhi kwa kutambua agizo la Mheshimiwa Rais la ujenzi wa Kiwanda cha Sukari kule maeneo yetu ya Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Waziri pengine atuambie Serikali imeandaa mpango gani kwa ajili ya matumizi ya ekari 150,000 ambazo zinaandaliwa baada ya ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme la Mwalimu Nyerere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Mheshimiwa Mchengerwa anajenga hoja, amesema alitarajia kwamba swali hili lingejibiwa na Wizara ya Ardhi, lakini wanufaika ni vile vijiji ambavyo amevitaja ambapo sisi kama TAMISEMI tuna maslahi na vijiji vile. Katika swali lake la nyongeza anataka kujua mpango wa Serikali wa matumizi ya ekari 50,000 baada ya ujenzi wa bwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii imekuwa makini, imekuwa ikifuata taratibu zote na kuona namna gani tufanye kulingana na wakati husika. Tutaainisha baada ya kujiridhisha kwamba eneo hilo litafaa kwa ajili ya shughuli gani na Mheshimiwa Mbunge naye atapata taarifa pamoja na wananchi wanaozunguka eneo la bwawa hilo.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuongezea kidogo katika suala hilo la kuendeleza Bonde la Mto Rufiji hekta 150,000 zilizokuwa downstream baada ya Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari tumeshaielekeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na imeshaanza kuainisha na kwenda huko kufanya utafiti kuonesha namna gani tutaanza kutumia kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji baada ya bwawa lile kumalizika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge aendelee kushirikiana na Serikali yake hii na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na sasa hivi tumeweka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji mpaka ngazi ya Wilaya. Kwa hiyo, kuna Afisa wa Tume ya Umwagiliaji kwenye Wilaya ya Rufiji, Mkoa wa Pwani, Kanda ya Mashariki pamoja na Taifa. Kwa timu hiyo, tutaenda kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ambacho ni kilimo cha uhakika.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya vikwazo ambavyo wanakutana navyo wawekezaji wengi hapa nchini ni urasimu na mchakato mrefu unaochukua muda mrefu wa kupata vibali vya kuwekeza katika maeneo mbalimbali; na mara nyingi Serikali imekuwa ikisema kwamba, inaendelea kuona namna gani inapunguza urasimu huo. Je, ni hatua gani imefikiwa kupunguza urasimu huu ili wawekezaji wanapokuja wasikutane na hivyo vikwazo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ambazo zimechukuliwa na Serikali ni dhahiri. Kwanza Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha Wizara mahususi kwa ajili ya kushughulikia suala la uwekezaji kulikoni ilivyokuwa zamani, ilikuwa haijulikani hasa suala hili liko wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzisha Wizara ambayo inashughulikia uwekezaji na maelekezo na miongozo ambayo imekuwa ikitolewa na yeye mwenyewe Mheshimiwa Rais na Viongozi wengine Wakuu wa Kitaifa kwamba, tupunguze urasimu ili tuweze kuvutia uwekezaji, naamini itatuondoa katika hali ya urasimu uliokuwepo na uwekezaji utachukua tija kwa muda mfupi zaidi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongezea majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwanza kabisa napenda tu kusema kwamba anayoyasema Mheshimiwa Mbunge ni kweli, lakini pia ninachosema ni kwamba tumebadilika sana ndani ya Serikali, lakini pia katika mamlaka zetu za Serikali za Mitaa. Moja, ambalo tunalifanya hivi sasa, kwanza ni kufanya mabadiliko na mapitio ya Sera yetu ya Uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tayari kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Wizara mbalimbali na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, tunavyoongea hivi sasa tayari timu iko kazini, inafanya marekebisho ya maeneo mbalimbali ambayo yamekuwa yakionekana ni vikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, tunashukuru sana Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI yenyewe, tayari tumeshaanza kuanzisha ofisi za kusaidia wawekezaji kupitia Regional Investiment Facilitation. Tayari Arusha wako katika hatua hiyo, tayari Iringa wameshaanza na tunaendelea kufanya hivyo katika mikoa mingine. Pia tunaandaa mwongozo ili mikoa yetu na mamlaka za Serikali za Mitaa ziweze kuwahudumia vizuri zaidi wawekezaji wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tunaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na tunaamini vikwazo vyote na mifumo mbalimbali ya udhibiti kupitia mamlaka zetu itaondolewa.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa naangalia kwenye haya majibu ya Serikali naona wametenga pesa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali, lakini pamoja na vituo vya afya, lakini kwenye majibu haya sijaona pesa ambayo imetengwa kwa mwaka 2019/2020 kwa ajili ya maboma ambayo yako mengi sana sehemu mbalimbali ambayo wananchi wamejitolea nguvu zao kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo hasa ya zahanati, ujenzi wa zahanati.

Mheshimiwa Spika, sijui Serikali ina mpango gani wa kusaidia kukamilisha ujenzi wa maboma mbalimbali ambayo yamo katika sehemu mbalimbali za majimbo yetu? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Tabora Manispaa jengo la Halmashauri limechakaa sana mpaka linavuja, sehemu nyingi zinavuja, lakini Halmashauri kwa mapato yake ya ndani imejitahidi kuligharamia jengo hilo na imelipa mpaka sasa hivi zaidi ya shilingi bilioni 1.5 kwa mapato ya ndani na toka ujenzi umeanza mwaka 2014 Serikali imewahi kutoa shilingi milioni 450 tu katika kusaidia ujenzi wa jengo hilo. Sasa sijui Serikali ina mkakati gani wa kusaidia ujenzi wa jengo hilo ambalo ujenzi wake unafikia shilingi bilioni tano ambayo kwa mapato ya Halmashauri kama ya Tabora Mjini si rahisi kukamilisha, Serikali ina mkakati gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la mwanzo anauliza haoni fedha ambazo Serikali imetenga kwa ajili ya kumalizia maboma ambayo wananchi wametumia nguvu katika kuyajenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, msingi wa majibu katika majibu yangu ya msingi yametokana na swali alilouliza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu katika swali lake la msingi ni kama vile hakuona jitihada ambazo zinafanywa na Serikali katika kuhakikisha ujenzi wa vituo vya afya, hospitali pamoja na zahanati na ndiyo maana katika majibu ambayo nimempa nimeonesha idadi ya fedha ambazo zimetolewa na Serikali na nia njema ya Serikali ambayo inaongozwa na CCM na sisi katika Ilani yetu tumeahidi pale ambapo wananchi wanatoa nguvu yao na Serikali tunapeleka mkono kusaidiana na wananchi ili kuhakikisha nguvu ya wananchi haipotei na yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge ni shuhuda nguvu kubwa ambayo inapelekwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili kuhusiana na ujenzi pale Manispaa ya Tabora ambao unatakiwa ugharimu kama kiasi cha bilioni tano ni ukweli jengo limeanzishwa ni kubwa kweli kweli na katika hali ya kawaida kwa bajeti ya Serikali inavyotengwa si rahisi kwamba jengo hili litakamilika lote kwa mara moja na ndiyo maana tumekuwa tukiwashauri ni vizuri tukaanza upande ambao tunaweza tukaukamilisha ukaanza kutumika wakati ujenzi mwingine unaendelea kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa Serikali kuvifanyia matengenezo barabara zote ambazo zimeulizwa kwenye swali hili, lakini kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019, barabara ya Kibaya Urughu imeharibika sana kwa sababu ya mvua, je, Serikali inasema nini kuhusu matengenezo ya barabara hiyo?

Mheshimiwa Spika, Swali la pili barabara zilizopo katika Jimbo la Mheshimiwa Mlata Singida zinafanana sana na barabara za Wilaya ya Chunya, bahati mbaya kwa miaka miwili mfululizo huko Chunya, TARURA hawajafanya kazi yoyote kuzitengeneza barabara za vijijini, hasa hasa barabara ya kutoka Chunya kwenda Soweto; Isenyela kwenda Sangambi; Kiwanja kwenda Ifumbo; Chunya kwenda Mapogolo; Lupa kwenda Lualaje; Chunya kwenda Sangambi, lakini kubwa kuliko zote barabara ya kutoka Sangambi kwenda Chunya ni mahandaki haipitiki kabisa, je, Serikali inasema nini kuhusu matengenezo ya barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anaongelea eneo la Urughu ambalo barabara imeharibika kutokana na mvua nyingi ambazo zimenyesha, ni ukweli usiopingika kwamba pale ambapo mvua zinanyesha nyingi na hasa katika barabara ambazo zinatengenezwa kwa kiwango cha vumbi ni uhakika kwamba kunakuwa na uharibifu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri tukawasiliana na Mheshimiwa Mbunge ili tukajua ukubwa wa tatizo ili tuweze kutoa maelekezo kwa TARURA ili matengenezo ya dharura yaweze kufanyika ili barabara hii iendelee kupitika kipindi chote, wananchi waendelee kupata huduma na kufanya shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, lakini anaongelea katika jimbo lake ambalo anasema linafanana sana na swali la msingi na anaeleza kwamba katika jimbo lake TARURA haijafanya kazi yoyote kwa mwaka mzima. Hali kama hii hatujaipata pahali pengine popote, ni vizuri tukawasiliana na Mheshimiwa Mbunge tukajua hasa nini ambacho kimetokea hadi barabara isitengenezwe na hali bajeti imekuwa ikitengwa.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza niishukuru Serikali pale Rombo nina Kituo cha Afya kinaitwa Kituo cha Karume, tulipewa shilingi milioni 500 kwa hiyo ni kimekuwa kituo cha afya cha kisasa kabisa sasa hivi. Hata hivyo vipo vituo ambavyo havina kabisa vifaa vya hospitali, na tuna upungufu wa wahudumu wa afya takriban asilimia 58 ya wahudumu wanaotakiwa kuwepo?

Je, Serikali iko tayari kutusaidia ili vituo vingine hivi viweze kupata vifaa ili kusaidiana na ile hospitali ya wilaya katika kuhudumia wagonjwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema tuna shida kubwa sana ya watumishi wa afya; asilimia 58 ya watumishi wanaotakiwa wawepo, hawapo, je katika mgao Serikali iko tayari kufikiria kutupatia mgao wa watumishi wa afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Joseph Roman Selasini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa wa niaba ya Wizara nipokee pongezi, Mheshimiwa Selasini anasema kituo chake ambacho amepata jumla ya shilingi milioni 500, ni miongoni mwa vituo vya kisasa kabisa nchini. Naomba nitumie fursa hii kuwataarifu Waheshimiwa Wabunge Vituo kama hicho anachokisema Mheshimiwa Selasini viko vimejengwa nchini nzima. Kwa hiyo ni pongezi ambayo inatustahili Serikali kuweza kuipokea kwa sababu ni kazi kubwa ambayo imefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake anaongelea suala zima la vifaa; naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine wote ambao vituo vya afya vimejengwa kwenye maeneo yao, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba vile vituo vyote ambavyo vimejengwa havibaki vikawa ni mapambo, vinatakiwa vikamilike na vipelekewe na vifaa. Hivi ninavyoongea kuna kiasi cha fedha takribani bilioni 40 ambazo tunazifatilia Hazina ili tuweze kuhakikisha kwamba vifaa vinanunuliwa na vinapelekwa vituo vyote vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, anaongelea juu ya umuhimu wa watumishi. Ni kweli, tukiweka vifaa bila kuwa na watumishi napo itukuwa hatujafanya lolote. Naomba nitumie fursa hii kumtaarifu yeye pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote kwamba katika maombi tumeomba kupatiwa watumishi 12,000 na ni imani yetu kwamba maeneo yatakayozingatiwa ni yale ambayo yana upungufu mkubwa ikiwa ni pamoja na maeneo ambayo ameyataja Mheshimiwa Roman Selasini.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi katika Ilani yake ilieleza kwamba itatoa matibabu bure kwa wazee, kwa Wilaya ya Nyang’hwale kuna wazee takribani 6,000 na wazee hawa ni 100 tu ambao wanapata matibabu bure, Je, Waziri ananiambia nini? Hawa wazee 5,900 waliobaki watapata vitambulisho vya kuweza kupata matibabu bure?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amar kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza, naomba tukubaliane naye kwamba si wazee wote ambao tumeahidi kuwapa matibabu bure, tumeahidi kutoa matibabu bure kwa wale wazee ambao hawana uwezo, kwa hiyo hilo lazima tuwekane sawa. Na ni ahadi ambayo iko thabiti baada ya kufata procedure zote ambazo zinatakiwa tunaamini kabisa wazee hawa wamefanya kazi kubwa katika kutumikia taifa hili la Tanzania ndiyo wametufikisha hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba wale wote ambao hawana uwezo wanatibiwa bure kama ambavyo sera ya Serikali inavyoelekeza. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Tuna Zahanati iko katika Kata ya Luhunga Kijiji cha Igoda, ile zahanati tulishamaliza kujenga kila kitu na vitanda tulishaweka, na sasa ina miaka miwili haijafunguliwa. Je, ni lini Serikali sasa itaenda kufungua ile zahanati ambayo imejengwa na wananchi ili iweze kuanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kutoa maelekezo kwa Waganga wote wa wilaya nchini, kwamba maeneo ambayo wananchi wamejenga zahanati na zimekamilika hakuna sababu ya kuendelea kusubiria zisianze kutoa huduma; na hasa pale anaposema Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari vifaa vyote vipo. Kwa hiyo ni vizuri ndani ya Wilaya wahakikishe kwamba wanapeleka watumishi; kazi ambayo inawezekana kabisa; ili zahanati hiyo ianze kufanya kazi na wananchi wafaidi matunda ya jasho lao.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kutokana na vyanzo vyetu vya fedha na kutokana na mipango kazi iliyopo, je, ni lini hasa Serikali inafikiri barabara hii itafanyiwa kazi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; barabara hii inahusisha uwekaji wa makalavati kadhaa. Je, Serikali haioni kwamba ni vema basi kutokana na vyanzo vya fedha vilivyopo, kazi zikagawanywa katika makundi kwamba labda itengenezwe barabara kwanza na makalavati baadaye au makalavati kwanza barabara baadaye, Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi, nimeonesha mpaka kiasi cha fedha ambazo zinatakiwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa, naomba nirudie ni shilingi milioni 288.9. Tafsiri yake ni kwamba tayari tumeshabaini hata vivuko vinavyotakiwa kuwekwa na kutengeneza barabara.

Mheshimiwa Spika, pia kwa wakazi wa Dodoma na Waheshimiwa Wabunge wa Dodoma, naomba niwaondoe hofu kama kuna sehemu ambayo Serikali imeamua kuwekeza kuhakikisha kwamba miundombinu ipo ya uhakika ni pamoja na Dodoma. Hivi karibuni ukitafuta kwenye bajeti hutaiona lakini kuna jumla ya kama shilingi bilioni 84 tumeamua kuwekeza kuhakikisha kwamba ring road zinaanza kujengwa immediately.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami naomba niulize swali dogo la nyongeza, kwanza nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri ambayo inafanya kukamilisha Vituo vya Afya ambavyo mimi mwenyewe kama Mjumbe wa Kamati hiyo nimejionea kwa macho yangu mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu sasa, kwa kuwa Kituo cha Afya Simbo kimekamilika na bado hakijaanza kazi, je, ni lini sasa hivyo vifaa tiba vitapelekwa haraka sana ili kuwapunguzia adha wagonjwa ambao wanakimbilia kwenda Hospitali ya Private ya Nkinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchemba, Makamu Mwenyekiti wa Kamati yetu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu nipokee pongezi kwa niaba ya Wizara na yeye mwenyewe amekuwa shuhuda amejionea kwa macho yake, lakini katika swali lake anauliza lini Kituo cha Afya hicho ambacho kimeshakamilika kitaanza kutoa huduma kama ambavyo Serikali imekusudia. Naomba nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge tayari fedha tumeshalipa MSD na vifaa vinanunuliwa moja kwa moja kutoka mtengenezaji, kwa hiyo wakati wowote vifaa vikishakamilika, lakini pia kumekuwa na changamoto ya Wataalam wa kutoa tiba kwa ajili ya usingizi anesthesia, tayari wamepelekwa Bugando mmoja na mwingine amepelekwa Muhimbili ili vifaa vitakapofika na wataalam waweze kutoa huduma ili wananchi wasihangaike kutembea umbali mrefu. (Makofi)