Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Tunza Issa Malapo (55 total)

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba Mheshimiwa Waziri aniambie ni lini ujenzi huo utaanza? Kwa sababu barabara hii imekuwa ikizungumzwa kwa muda mrefu. (Makofi)
Swali la pili; issue hapo ni ku-sign mkataba ama ni pesa? Kwasababu tumekaa kwenye kikao cha RCC ingawa Meneja wa TANROADS Mkoa alishindwa kusema wazi, lakini kinachoonekana pesa hakuna. Kwahiyo, issue ya msingi naomba kujua; ni kwamba mkataba haujasainiwa ama pesa zinazofanya mkataba usainiwe hazipo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Tunza Issa Malapo, kwa niaba ya Wabunge wote wa Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu walikuwa na kikao cha RCC na walikataa kuijadili barabara hii wakataka ije ijadiliwe hapa Bungeni. Naomba nikuhakikishie, hamna sababu ya kuijadili hapa Bungeni. Barabara hii imetengewa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2016/2017 barabara hii imetengewa fedha tutakayohakikisha hizo kilometa 50 zinajengwa. Tunachosubiri ni taratibu za mkandarasi ku-sign mkataba kukamilishwa. Fedha zimetengwa!
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kutoa masahihisho, Naibu Waziri wakati anajibu aliniita Malopo naitwa Malapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, je, Serikali iko tayari sasa kuwaambia wananchi kuwa haiko tayari kutekeleza Sera ya Elimu Bure kwa maana halisi ya Kiswahili ya neno bure isipokuwa elimu inayotolewa sasa ni ya kuchangia gharama? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nini wito wa Serikali kwa wananchi kuhusu sera hii ili kuwawezesha walimu kufanya kazi yao bila kero kutoka kwa wazazi wanaofikiri hawawajibiki kulipa pesa yoyote kwa ajili ya elimu hiyo kwa watoto wao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante. Kwanza naomba radhi kwa kukosea jina la Mheshimiwa Mbunge ni Malapo na nakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala kwamba Serikali iseme haina nia ya dhati katika suala zima la elimu bure, ndugu zangu naomba niwaambie, kama sisi ni mashahidi wa kweli vijana wengi waliokuwa wanaenda sekondari walikuwa wanashindwa kulipa hizi gharama za kawaida. Hata wale waliokuwa wanaanza elimu ya msingi mnafahamu wazazi wengi sana wanashindwa kulipa zile gharama za awali ili mtoto wake aweze kujiunga na shule na ninyi wenyewe ni mashahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi juzi kupitia vyombo vya habari wazazi wanakiri kabisa kwamba suala hili limewasaidia kwa kiwango kikubwa vijana wao kwenda shule. Hata turn over katika shule zetu imekuwaje? Hata madarasa wakati mwingine shule zinahemewa kwa sababu wazazi wote ambao mwanzo walikuwa wanakwazika na gharama hizi sasa wanapata fursa ya kuwapeleka watoto wao shule. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tukiri kwamba Serikali katika hili imefanya juhudi kubwa sana. Naamini jambo lolote lazima lina changamoto zake, hizi changamoto ndogo-ndogo ni kwa ajili ya kuboresha ili mradi mpango uende vizuri lakini dhana ya Serikali imekamilika na inaenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika sehemu ya pili, wito wa Serikali Walimu wasibughudhi wazazi, nadhani tumeshasema wazi na Waziri wangu jana alilisema wazi kwamba jambo kubwa elimu hii ni bure. Hatutarajii mwalimu awazuie watoto kwenda shule kwa kuzusha mchango wake mwenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili tumesema tutakuwa wakali sana kwani lengo kubwa ni mtoto wa Kitanzania aweze kupata elimu ya shule ya msingi na ya sekondari mpaka form four. Lengo ni kwamba kila mwanafunzi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania apate fursa ya uongozi na mikakati ya Serikali ya Awamu ya Tano.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAMISEMI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuongezea majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri wa TAMISEMI kutokana na maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Malapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imefanya jitihada kubwa katika suala hili la elimu bure, lakini inasikitishwa kwamba wenzetu walihoji fedha hizi zimetoka wapi kwenye bajeti na leo fedha hii iliyotolewa kwa ajili ya kusaidia jamii maskini watoto wao waende shule wanahoji tena hiyo bure gani, ni mkanganyiko ambao haueleweki. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAMISEMI): Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme tu, katika kila shule za msingi za kutwa tutapeleka kila mwezi shilingi 600/= kwa kila mtoto kwa ajili ya uendeshaji. Kwa shule za sekondari za kutwa tunapeleka kwa kila mwezi shilingi 3,540.57/= kwa kila mtoto kwa ajili ya uendeshaji wa shule. Kwa wale wa bweni tunapeleka shilingi 7,243.39/= kwa kila mwezi. Fedha hizi zikijumlishwa uwezekano wa kuendesha elimu upo pamoja na changamoto zilizopo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ninavyozungumza kutokana na mpango huu wa elimu msingi bila malipo pale ambapo tulitegemea wajiandikishwe watoto 80 kuanza darasa la kwanza wamejiandikisha 240; pale tulipotaka wajiandikishe watoto 180 wamejiandikisha karibu 700 na hiyo ni Dar es Salaam tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, yako baadhi ya maeneo uwezekano tu wa kuwapokea watoto hawa ni mgumu kwa sababu wazazi maskini wameona mpango huu ni muhimu kwao na umewasaidia sana.
Kwa hiyo, kuubezabeza hapa ni kwenda kinyume kabisa na wananchi ambao wanaona mpango huu umewasaidia na kwa hakika kusema kweli unalisaidia Taifa. Tupingane katika mengine lakini kwenye jambo zuri tutiane moyo kama Watanzania. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa vile Waziri amekiri kwamba, miradi mingi ya umwagiliaji ilikuwa na matatizo sasa je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu wakandarasi na wote waliohusika kufanya ubadhirifu wa pesa hizo nyingi, hasa ukizingatia kuna mradi wa umwagiliaji kule Kitele, Jimbo la Mtwara Vijijini mkoani Mtwara, ambalo kwa kweli wananchi walijitolea eneo lao, lakini mradi umejengwa chini ya kiwango, mifereji ina nyufa
na ule mradi haujaanza kutumika. Nini kauli ya Serikli kuhusu miradi hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa
Naibu Spika, kama nilivyosema hii miradi tunaifanyia mapitio, lakini pale itakapoonekana mkandarasi au kuna mtu yeyote amefanya ubadhirifu, Serikali itachukua hatua zinazostahiki kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, naomba asiwe na wasiwasi, lakini lengo kubwa hasa la Serikali ni kuhakikisha kwamba miradi hii tunaikamilisha ifanye kazi iliyokusudiwa kwa wananchi.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Baada ya kupandishwa hadhi Zahanati ya Likombe katika Manispaa ya Mtwara Mikindani kuwa Hospitali ya Wilaya kumekuwa na changamoto kubwa sana ya mrundikano wa wagonjwa hasa katika wodi ya wazazi. Je, ni lini Serikali itapanua wodi ile ili akinamama wale waweze kusitirika wakati wanatimiza haki yao ya msingi kama wanawake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, population ya Mtwara Mikindani sasa hivi imekuwa kubwa kutokana na kuingiliana na mambo ya gesi. Hata hivyo, hivi sasa tunaenda katika harakati za kufanya ukarabati wa vituo vipatavyo 142. Zoezi hili haliishi hapa; Serikali inajielekeza tena kupanua vituo vingine vipya ambako kuna population kubwa. Kituo hiki ambacho Mheshimiwa Mbunge amekizungumzia hapa tutakichukua kama sehemu ya kipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kufanya commitment katika kuwahudumia wananchi. Kwa hiyo, hii tutaweka ni sehemu ya kipaumbele kuwahudumia wananchi wa Mikindani ili waweze kupata afya bora katika maeneo yao.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kutokana na ripoti ya CAG mpaka sasa hivi inaonekana ni 6% tu ya gesi inatumika, inayosafirishwa na hilo bomba na uwekezaji huu ni wa pesa nyingi. Nataka kujua Serikali imejipanga vipi kuhakikisha uwekezaji huu unaleta tija kwa Taifa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kuna utata mkubwa katika uwekezaji huu kujua gharama halisi: Je, Serikali ipo tayari kumtaka CAG afanye special audit katika uwekezaji huu? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwanza bomba la kusafirisha mafuta au gesi kwa sasa kutoka Madimba (Mtwara) hadi Dar es Salaam ndiyo bomba kubwa tulilonalo kwa upande wa gesi.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa sasa hivi gesi inayosafirishwa ni kati ya 6% hadi 10% ya uwezo wake na uwezo nimetaja ni milioni cubic feet 744. Sasa ni kwa nini? Bomba hilo lina upana wa inchi 36, ni kubwa; na mahitaji ya sasa ni megawati 668 tulizonazo kwa upande wa gesi, lakini miundombinu inayojengwa ndiyo mikakati sasa.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa tunajenga miradi miwili ya kusafirisha gesi Kinyerezi I na Kinyerezi II. Kinyerezi I tunafanya extension ya kuongeza megawati 185 ili katika Kinyerezi I pekee zifikie 335.
Mheshimiwa Spika, kadhalika tunajenga mradi mwingine katika Kinyerezi II ambao utaweza kutoa megawati 240. Sasa miradi hii miwili ikikamilika, mahitaji makubwa ya gesi yataongezeka. Kwa hiyo, itazidi 6% hadi 10% na tuna matarajio inaweza kufikia asilimia 20 hadi 30.
Mheshimiwa Spika, miundombinu inayojengwa kuhitaji gesi, bado ni mingi; tunahitaji umeme wa kutosha. Kwa sasa hivi umeme hautoshi. Ni matarajio yetu kwamba mara baada ya miradi mingine, tutakwenda Kinyerezi III utakaoanza mwaka 2018 utakaohitaji megawati 600. Kwa hiyo, mahitaji ya gesi bado yatakuwa ni makubwa.

Mheshimiwa Spika, lingine niseme mkakati mwingine, unapokuwa na gesi ya kutosha inakuruhusu kujenga miundombinu mingine kwa sababu una stock. Kwa hiyo, siyo hasara kuwa na gesi nyingi lakini kadhalika mikakati ya Serikali ni kuhakikisha kwamba hii gesi tunasafirisha kadri iwezekanavyo ili ichangie sana katika upatikanaji wa umeme. Mkakati wa Serikali ni kutumia gesi zaidi ili kuachana na mafuta ili kuwapunguzia mzigo wananchi, hilo ni katika ufafanuzi wa swali la kwanza.
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ukaguzi, mahesabu ya Serikali hukaguliwa mara kwa mara, ni utaratibu wa kawaida. Kama ambavyo kila mwaka CAG hukagua, hata miradi hii ataendelea kuikagua.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu, suala la ukaguzi wa miradi ni endelevu, CAG ataendelea kukagua ili hali halisi iendelee kufahamika.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
(a) Naomba anieleze ni tatizo gani linalofanya Mji huu usipate maji ya kutosha na ya uhakika wakati vyanzo vya maji vipo?
(b) Pia ni lini wananchi hawa walioteseka kwa muda mrefu hasa wanawake watapata maji safi na salama? Nataka time frame, ni lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni matatizo gani yanafanya wananchi hawa wasipate maji. Ni kweli kabisa kwa bahati nzuri Mheshimiwa Mbunge ni shahidi, katika Mikoa na Wilaya ambayo nilitembelea ni pamoja na Wilaya ya Nanyamba. Maeneo yale yana vyanzo vikubwa vya maji vya Mitema na Mkunya. Tatizo ni kwamba huko nyuma tulikotoka upatikanaji wa fedha ulikuwa kidogo siyo mzuri na kwa sababu tumekuwa tunaishi kwa kutegemea wafadhili vile vile. Hilo ndilo ambalo limefanya miradi ile isiweze kukamilika na kutoa maji yale yanayotakiwa kwa matumizi ya wananchi wa Nanyamba.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ameuliza ni lini. Sasa hivi tumeingia kwenye program ya pili ya maendeleo ya maji ambayo tunatarajia Serikali inatenga fedha na tunaanza kutenga fedha kuanzia mwaka ujao wa fedha, pia wafadhili wametuahidi na kuna juhudi kubwa ambayo inafanywa na Serikali kupitia Waziri wa Fedha, lakini na Mwanasheria wa Serikali pia ambapo tunaongea na wafadhili waweze kutupatia pesa ili tuweze kukamilisha hii miradi ya Mito ya Mitema na Nanyamba ambayo itahakikisha kwamba vyanzo vya Mitema na Mkunya ili tuweze kuhakikisha maji yanapatikana kwa hizi Wilaya za Nanyamba pamoja na Tandahimba.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, wamesema wanaajiri walimu wa sayansi, hisabati na kadhalika, lakini bado tatizo la walimu hao ni kubwa. Nataka kujua tu, wamefanya sensa, ni walimu wangapi wa sayansi ambao kila siku wanaacha kazi kwa sababu ya maslahi duni katika Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili ni gumu sana, kwa sababu hatuna takwimu za kila mwaka kwamba ni walimu wangapi wa sayansi na hisabati wanaacha kazi.
Lakini comfort niliyonayo na ambayo nataka niwape Waheshimiwa Wabunge ni kwamba malalamiko tuliyonayo ni ya walimu kutaka kuhama haraka katika shule wanazopelekwa, yaani mwalimu anaweza akapelekwa kwenye shule fulani, akikaa baada ya wiki mbili anataka ahame. Hiyo ndiyo changamoto kubwa tuliyonayo ambayo tunaishughulikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuacha kazi, hilo naomba sana tutoe majibu baadae.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Chama cha Mapinduzi kimeshindwa kuendeleza viwanja vingi vya michezo, ikiwemo kiwanja cha Nangwanda Sijaona katika Manispaaa ya Mtwara Mikindani.
Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kurudisha viwanja hivyo Halmashauri kama ilivyofanya kwenye mashamba yasiyoendelezwa ya watu binafsi? (Makofi)
Swali langu la pili, kwa kuwa michezo ni afya, michezo ni ajira, na michezo ni furaha. Kwa kuwa chama cha Mapinduzi kimeshindwa kuviendeleza viwanja hivi na kuwafanya wanamichezo wetu wacheze katika mazingira duni...
Mheshimiwa Spika, naomba unisikilize. Michezo ni afya, ni furaha na ni ajira. Kwa kuwa, Chama cha Mapinduzi kimeshindwa kuviendeleza viwanja hivi hatuoni kwamba Chama cha Mapinduzi kina nia ya kudunisha wanamichezo wetu kwa sababu wanapata ajali mbalimbali wanapokuwa wanachezea katika viwanja hivyo? Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nikuhakikishie kupitia Bunge lako tukufu kwamba, siyo kweli kwamba CCM imeshindwa kwa sababu asilimia 99 ya michezo yote nchini inaendeshwa kwenye viwanja hivyo, sasa kushindwa huko kukoje? Sasa hivi tunaanza Ligi Kuu ya Tanzania na sehemu kubwa ya michezo hiyo itachezwa kwenye viwanja hivyo hivyo.
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na wewe kwamba vingi haviko kwenye hali nzuri sana na Wizara ilikuwa imeiachia Shirikisho la Soka nchini kufanya majadiliano na wenye viwanja, sasa tumeona maendeleo siyo ya kasi ya kutosha, Wizara imeamua yenyewe sasa siyo tu kwa kushirikisha Shirikisho la Soka nchini, mashirikisho yote ya michezo nchini, kukaa pamoja na wamiliki tuweze kukubaliana namna ya kuboresha hivi viwanja na kuweza kupata misaada ambayo kwa kawaida itakwenda kwa urahisi zaidi kwa taasisi ambazo zina ubia na Serikali. Tunataka watuachie ubia wawe na ubia na Serikali ili tuweze kurabati viwanja, kama ambavo FIFA ilivyoweza kukarabati Kiwanja cha Kaitaba na Kiwanja cha Nyamagana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali imekiri kwamba mitambo ni michakavu na ni kweli ni ya muda mrefu; je, imejipangaje kununua mitambo mipya ulizingatia kuna ongezeko kubwa la mahitaji ya umeme katika mikoa hiyo ya Lindi na Mtwara?
Swali la pili; ni lini Serikali itaunganisha mfumo wa gesi asilia ili uweze kutumika katika majumba ya Mkoa wa Lindi na Mtwara ukizingatia kwamba kule ndiko gesi inakozalishwa? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Tunza Malapo kwa kufuatilia masuala ya umeme katika Mkoa wa Mtwara. Kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya swali la msingi; kwanza, Serikali baada ya kuona uchakavu wa mitambo hii tisa ya Kituo cha Mtwara, imenunua mitambo miwili mipya. Hivi ninavyozungumza, kazi ya ufungaji wa mitambo hii inaendelea ambayo itazalisha megawati nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua Mikoa ya Mtwara na Lindi mahitaji yanaongezeka, Serikali imekuja na mpango wa kujenga mitambo mingine ya kuzalisha umeme megawati 300 kwa kutumia gesi na mpaka sasa Kampuni ya JICA imeendelea na upembuzi yakinifu. Kama ambavyo tumesema kwenye bajeti yetu mradi huu utaanza kutekelezwa mwaka 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimtoe wasi wasi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeliona hilo na kwamba mradi huu mkubwa wa megawati 300 utatatua matatizo yote katika Mikoa hiyo ya Kusini na pia itaupeleka umeme katika Gridi ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameeleza ni lini mpango wa kusambaza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Tunza ameulizia ni lini mpango wa kusambaza gesi asilia majumbani katika Mkoa wa Mtwara utaanza? Napenda nimthibitishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kama ambavyo ameona hivi karibuni tumezindua mpango wa kusambaza gesi asilia katika Mkoa wa Dar es Salaam, lakini Mkoa wa Dar es Salaam unakwenda sambamba na Mikoa ya Mtwara na Lindi. Kwa hiyo, hii kazi itafanyika katika mwaka 2018/2019, tutasambaza gesi katika maeneo mbalimbali kwa matumizi ya majumbani kwa Mikoa hiyo. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawaili ya nyongeza. Swali la kwanza; katika Manispaa ya Mtwara Mikindani tatizo kubwa ni miundombinu ya usambazaji wa maji, maji yapo, lakini miundombinu ndilo tatizo. Namuuliza Mheshimiwa Waziri ni lini miundombinu ile itaboreshwa, ili kusudi zile kata za pembezoni zipate maji ya uhakika? Maana tumekuwa tukiliongea suala hili siku nyingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kumekuwa na kero, watumiaji wa maji katika Manispaa ya Mtwara Mikindani wanalalamika kwamba, wanabambikiwa bill na hiyo inatokana na mamlaka kushindwa kusoma bill katika nyumba zote kutokana na ufinyu wa wafanyakazi. Je, Mheshimiwa Waziri, anatambua kama kuna ufinyu wa wafanyakazi katika mamlaka na kuna jitihada gani za kuhakikisha wanapatikana wafanyakazi wa kutosha? Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtaarifa Mheshimiwa Mbunge tu kwamba tumesaini mkataba wa shilingi bilioni tano kwenye Mamlaka ya Maji ya Mtwara ambayo katika huo mradi utaongeza vyanzo lakini pamoja na miundombinu ya kusambaza maji katika Mji wa Mtwara na hiyo ni hatua ya kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na usomaji wa bills kwenye nyumba za watu tayari sasa hivi malalamiko yaliyokuwepo baada ya muda mfupi, yatakwisha kwa sababu, sasa tunatumia teknolojia mahususi ambayo kwanza hakutakuwa na mtu kuzidishiwa bill. Ni kwamba, zile mita zitasoma unit baada ya maji kupita sio baada ya hewa kupita, kwa hiyo, suala hilo Mheshimiwa Mbunge tutalimaliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo Mheshimiwa Mbunge Ilani ya Chama cha Mapinduzi tayari itatekeleza mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka Mto Ruvuma ambao utaleta maji Mjini Mtwara na baada ya hapo Mji wa Mtwara hautakuwa na tatizo tena la maji, maji yatakuwa mengi, yatahudumia maji ya majumbani pamoja na maji ya viwanda. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira tu, Serikali yake ya Chama cha Mapinduzi inafanyia kazi hili na tayari baada ya muda mfupi utekelezaji wa mradi huo mkubwa utaanza.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Mwambe nina maswali mawili ya nyongeza.
La kwanza, kuna taarifa kwamba mkandarasi ambaye amepewa kazi ya kukamilisha miradi hii ya REA katika Mkoa wa Mtwara, hasa Wilaya ya Masasi yenye Jimbo la Ndanda pamoja na Nanyumbu ana matatizo ya kiusajili.
Je, Serikali haioni ni wakati mwafaka wa kuachana na mkandarasi huyu na kumtafuta mwingine ambaye atakamilisha kazi hii kwa wakati? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, umeme ni huduma, lakini pia umeme ni biashara. Inakuaje mji mpya unapoanzishwa watu wamekaa wanahitaji huduma ya umeme lakini hawaipati kwa wakati? Serikali mnahujumu shirika hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza kwa niaba ya Mheshimiwa Cecil Mwambe na swali lake la kwanza limejielekeza kwa Mkandarasi anayefanya Mradi huu wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza ambaye kwa mujibu wa jibu langu la msingi nimemtaja, JV RADI Services.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maelezo ya Mheshimiwa Mbunge, nataka nimthibitishie kwamba mkandarasi huyu siyo kwamba ana tatizo la usajili, ni utaratibu wa kawaida wa kuhakiki ambao upo ndani ya Serikali. Kuna jumla ya Wakandarasi sita katika Mradi huu wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza ambao uhakiki wao unaendelea kwa vyombo mbalimbali.
MheshimiwaMwenyekiti, kwa hiyo, naomba wakazi wa Mtwara wavute subira kwamba hivi karibuni tu uhakiki huo utakamilika na ataendelea na kazi. Sambamba na hilo, pamoja na uhakiki huo, huyu mkandarasi alipewa mkataba kwa mujibu wa taratibu, lakini pia ameanza kazi. Kuna vijiji kama vitatu Mtwara Vijijini amewasha umeme, anaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kwa maeneo ya miji ambayo inakua, Mheshimiwa Mbunge ameeleza kwamba upatikanaji wa umeme au uunganishwaji wa miundombinu ya umeme unakuwa ni shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge na kama ambavyo tumewasilisha bajeti yetu jana, kuna miradi mbalimbali ambayo Serikali imeona ianze kutekeleza ili kukidhi mahitaji ya umeme katika miji inayokua. Mfano, kuna mradi unaokuja peri-urban Awamu ya Kwanza utakaoanza mwaka wa fedha 2018/2019. Pia hata densification ya awamu ya pili ambayo ni kwa mikoa 11 ikiwemo Mtwara, Dodoma, Kagera, Singida, Lindi, Kilimanjaro, itaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali imeliona hilo kwa kuwa kazi ni nyingi na tumeona tuisaidie hilo liweze kuendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mimi nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali langu la kwanza; nataka tu kujua katika ile Hospitali ya Mkoa ya Ligula kuna Madaktari Bingwa wangapi na wanatibu magonjwa gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa hospitali ile ni ya mkoa, maana yake inahudumia mkoa mzima na ni ya rufaa na sisi hatuna hospitali ya kanda, Kanda ya Kusini, bado haijaanza kufanya kazi.

Katika jibu lake la msingi amesema Madaktari wa kufanya upasuaji wa kawaida na mifupa bado wapo masomoni wanasoma na ukizingatia kuna ajali nyingi zinazotokea, anawaambia nini vijana, wananchi wa Mtwara ambao wanapata matatizo, wanataka tiba ya upasuaji wa kawaida na mifupa; wasubiri mpaka mwaka 2021?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mtwara, Ligula tuna Daktari Bingwa mmoja katika Magonjwa ya Akinamama, lakini tunatambua kwamba tunahitaji huduma za Madaktari Bingwa katika hospitali zetu za rufaa za mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tulitangaza nafasi hizi Madaktari hawa hawako mtaani na ndiyo maana sisi kama Serikali tumewekeza katika kuhakikisha kwamba tunatoa mafunzo kwa Madaktari Bingwa wengi iwezekanavyo na tumeendelea sasa hata kufanya mabadiliko ya mifumo ya kufundisha Madaktari ili tuweze kupata Madaktari Bingwa wengi kwa utaratibu wa fellowship ambao na sisi ndani ya Wizara tunakwenda nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kwa lengo la kutibu changamoto ambazo tunazo Serikali imekuwa inafanya kambi mbalimbali za kutoa Madaktari Bingwa kutoka sehemu moja kwenda kwenye sehemu mbalimbali na hii tumekuwa tunafanya kwa kushirikiana na Bima ya Afya na kwenda katika kambi katika mikoa mbalimbali kuhakikisha kwamba zile huduma za dharura ambazo zinahitaji upasuaji nazo zinaweza zikafanyiwa kazi wakati tunasubiria kujenga uwezo wa kuwa na Madaktari Bingwa wengi zaidi.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Suala la kupandishwa madaraja linaambatana na ongezeko la mishahara. Serikali hii ya Awamu ya Tano imekuwa haipandishi watu madaraja kwa wakati, mtu anakaa mpaka miaka sita, saba, hajapandishwa madaraja. Nataka tu kujua Serikali iko tayari kuwalipa wale watu arrears zao kwa ile miaka ambayo hawakupandishwa madaraja kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri amesema wafanyakazi wafanye kazi kwa bidii. Hivi kweli anafikiri unaweza kumkamua ng’ombe maziwa kama humpi chakula cha kutosha? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba kipekee nimpongeze sana kwa jinsi ambavyo anafuatilia masuala yote ya watumishi wa umma nchini. Hata hivyo, naomba niseme kwamba, katika upandishwaji wa madaraja tuna madaraja ya aina tatu, kuna kupandishwa kwa madaraja kwa maana ya salary increase, kuna annual increment na kuna salary promotion, lakini katika suala la upandishwaji wa madaraja Serikali ilitoa tamko hapa wiki tatu zilizopita kwamba, kuanzia Mei Mosi mwaka huu (2019) Serikali inatarajia kupandisha madaraja, vyeo, watumishi zaidi ya 193,000. Hilo zoezi limeshaanza, lakini vilevile mwaka 2017/ 2018 Serikali ilishalipa annual increment zaidi ya bilioni 72.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile naomba niseme kabisa kwamba, Walimu walishalipwa zaidi ya bilioni 37, lakini kada nyingine za utumishi wa umma walishalipwa zaidi ya bilioni 35, lakini malimbikizo ya mishahara zaidi ya bilioni 75 zimelipwa. Isitoshe tu, lakini zaidi ya wastaafu waliokuwa wanaidai Serikali wameshalipwa zaidi ya bilioni tisa na hawa wastaafu ni zaidi ya 1,800.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili ni kwamba, Serikali inawajali sana watumishi. Sio lazima iwe katika nyongeza tu ya mshahara, lakini vilevile tukumbuke kwamba, Serikali ndio guarantor, watumishi wanapotaka kujenga nyumba, watumishi wanapotaka kufanya mikopo, kuna bima za afya zote hizo ni sehemu ya motisha. Kwa hiyo, naomba niseme kabisa Serikali inawajali watumishi katika njia mbalimbali na hata katika kupanda madaraja hiyo imeshaanza kutekelezwa. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, sijui mchakato utakamilika lini, lakini kuna mambo mawili; kunakuwepo mashine na kunakuwepo msomaji. Katika Hospitali hii ya Mkoa wa Mtwara kuna tatizo pia la msomaji wa x-ray, mtu amevunjika mkono sehemu ya nyuma, inaonekana amevunjika mkono sehemu ya mbele. Sasa nataka kujua Serikali imejipanga vipi inapopeleka hiyo mashine tena ya digital na kumpata mtu ambaye ataendana na hiyo mashine katika usomaji wake?

Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili, katika Hospitali ile ya Mkoa wa Mtwara kumekuwa na tatizo kubwa la madaktari hasa upande wa wanawake. Nataka kujua Serikali imejipanga vipi na ni lini itapeleka madaktari hao ili kutoa kero hii ambayo iko kwa muda mrefu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri na ufuatiliaji ambao anaufanya katika sekta hii ya afya na hususan katika Mkoa huu wa Mtwara. Labda niseme ni hivi kwamba katika hili eneo ambalo ameligusia kuna mambo mawili kuna suala la mpiga picha ambaye ni radiographer, yeye kazi yake ni kupiga picha, lakini tuna radiologist ambaye yeye ni msomaji wa picha. Digital x-ray tutafunga na ni kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, mashine ziko bandarini tunafanya utaratibu wa ugomboaji na tutaenda kuifunga pale Ligula, radiographer tunao.

Mheshimiwa Spika, suala la msomaji tunakuja na utaratibu mpya kwa sababu hii ni digital x-ray sisi kama Serikali na sisi tunaingia katika mfumo unaitwa telemedicine na tutakuja na kitu kinaitwa tele-radiology, kwamba hizi digital x-ray zote ambazo tunazifunga kwa kutumia Mkongo wa Taifa pale Muhimbili na pale MOI sasa hivi tumetengeneza kitu kinaitwa hub. Tutakuwa na centre moja ambayo kutakuwa na screen ambayo imeunganishwa na mtandao, picha zitakazopigwa Tanzania kote iwe ni Mbinga, iwe ni Ligula, iwe katika eneo lolote Tanzania hii zitakuwa zinatumwa, wataalam/madaktari wetu bingwa pale Muhimbili wataisoma ndani ya dakika 15 na lile jibu linarudi tena kulekule ambako linatoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikutoe mashaka sisi kama Serikali tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba matumizi ya hizi digital x-rays zinaweza zikatumika na wananchi wa Tanzania wananufaika na utaratibu mpya ambao tumeanza nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la pili la Madaktari Bingwa; ni kweli Hospitali ya Mkoa ya Ligula ina changamoto ya Madaktari Bingwa na sasa hivi sisi kama Serikali tunawekeza katika kuhakikisha kwamba hospitali za rufaa za mikoa ikiwa ni pamoja na Ligula tunakuwa na madaktari bingwa wa magonjwa ya wanawake, madaktari bingwa wa magonjwa ya ndani, madaktari bingwa wa magonjwa ya watoto, madaktari bingwa wa magonjwa ya mifupa, madaktari bingwa wa magonjwa ya dharura, pamoja na mengine mengi.

Kwa hiyo, sasa hivi wapo Madaktari wapo katika mfumo wa mafunzo na tumesomesha zaidi ya madaktari 100 kwa mwaka pale watakapokamilisha masomo yao tutawapangia katika hospitali zetu ya Iligula na hospitali zingine za RRH. Lengo na kusudio la Serikali wakati tunaboresha vituo vya afya, hospitali za wilaya, tunataka sasa hospitali za rufaa za mikoa zitoe huduma za kibingwa kama ilivyokusudiwa.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa bahati nzuri nimewahi kwenda mara kadhaa kwenye Mabaraza ya Kata. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri amesema Mwanasheria wa Halmashauri anasimamia Mabaraza hayo, lakini kiukweli kabisa hakuna usimamizi wa kisheria unaopatikana pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu: Je, Serikali iko tayari kuweka utaratibu mahsusi ili kusudi Mwanasheria apatikane wa kueleza na kuhakikisha wananchi wanatendewa haki kwa sababu unakuta Baraza la Kata linahukumu kesi ya shilingi milioni 10 wakati wao mwisho wao ni shilingi milioni tatu. Ni kwa sababu ya kukosa Mwanasheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua, Serikali imejipangaje kuhusu hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Siyo kweli kwamba Wanasheria hawasimamii haya Mabaraza ya Kata. Kama nilivyosema, kwenye majibu yangu yaliyotangulia hapa, kama kuna malalamiko kwenye eneo specific, Mheshimiwa Mbunge ni vizuri akataja ili tuweze kuchukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nina mfano. Kule Kivule tulikuwa na shida kwenye Baraza la Kata, tulimwita Mwanasheria wa Halmashauri ile ya Manispaa ya Ilala akaja akasikiliza malalamiko yaliyokuwepo, gharama kubwa ya uendeshaji wa kesi, uonevu na kuvuka kiwango ambacho kimewekwa kwa mujibu wa sheria, tulivunja Baraza tukaweka viongozi wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama kuna malalamiko katika eneo mahsusi tupewe taarifa. Vilevile tujue kwamba Wanasheria wako kwa mujibu wa Sheria hii ili haya Mabaraza ya Kata na yanaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya mwaka 1985 na imeendelea kufanyiwa marekebisho kadri muda unavyoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama kuna malalamiko, lazima tuchukue hatua. Hata hivyo, Mwanasheria wa Halmashauri ana uwezo, kwa sababu hazungumzi mtu mmoja, Idara ya Sheria kwenye Halmashauri ina wajibu huo. Ila kama kuna Mwanasheria kwenye Halmashauri yoyote hapa Tanzania, ameshindwa kufanya wajibu wake na haendi kila siku, Mbunge umepeleka malalamiko, wananchi wamelalamika, wamehukumu kesi kinyume na utaratibu, tupe taarifa tuweze kuchukua hatua kwa Mwanasheria huyo wakati wowote kuanzia sasa. Ahsante.

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa. Kwanza namshukuru Naibu Waziri, TAMISEMI kwa kujibu vizuri. Pia pamoja na hiyo aliyosema Naibu Waziri, changamoto hii kama Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pia tumeiona kwa sababu watu wale mashauri yao mengi yanahusiana na ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, Wizara yetu kwa kusaidiana na Msajili wa Mabaraza, akishirikiana na Wanasheria katika Halmashauri, tumeweka utaratibu wa kutoa mafunzo kwa zile Kamati zote za Mabaraza ya Ardhi ya Kata pamoja na Vijiji ili kuweza kuwapa elimu na ukomo wa namna wao wanavyotakiwa kusimamia. Kwa sababu wanapokwama, mashauri mengi yanaenda kwenye Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumeona kwamba tujenge msingi kule chini ili watu waweze kufanya kazi zao vizuri kwa weledi ili kupunguza malalamiko ambayo Waheshimiwa Wabunge wanayasema.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana katika Manispaa ya Mtwara Mikindani yaani Jimbo la Mtwara Mjini kumekuwa na tatizo kubwa la maji kutoka yenye tope jingi kwa muda mrefu na maji hayo yanapita katika mita za wananchi kuwasababishia kulipa bili wakati maji wanayoyapata ni machafu. Pamoja na mambo mengine chanzo kikubwa ni kukosekana kwa chujio katika chanzo cha maji cha Mtawanya.

Swali langu, ni lini Serikali itanunua chujio kubwa la uhakika kwa ajili ya kuchuja maji katika chanzo cha Mtawanya ili kusudi wananchi wanaoishi Mtwara Mikindani wapate maji safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji niseme kwa ufupi sana ni wajibu na ni haki ya mwananchi kupatiwa maji, si maji tu kwa maana yamaji safi na salama na yenye ubora. Nimefika Mtwara lakini moja ya changamoto kubwa pale ni chujio na nitumie nafasi hii kumwagiza Katibu Mkuu wa Wizara yetu ya Maji kuhakikisha mchakato ule unakamika haraka kwa ajili ya ujenzi wa chujio na wananchi wa Mtwara waweze kupata maji safi salama na yenye ubora. Ahsante sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuruku, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri uko tayari kunipatia mchanganuo wa hao wafanyakazi 7,000 wanaohitajika wanatosheleza kwa kiwango gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Swali langu la pili, kwa kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania ndiyo mamlaka iliyopewa wajibu mkubwa wa kukusanya kodi; na kwa kuwa ukirejea hotuba mbalimbali za Wizara ya Fedha utaona kuna upungufu mkubwa sana wa wafanyakazi; na kwa kuwa huko mtaani kuna vijana wengi ambao wamehitimu kwenye masuala mbalimbali ya kodi lakini hawajaajiriwa. Sasa nataka kujua, ni lini Serikali itaajiri Vijana wale ili wapate ajira na Mamlaka ifanye kazi kwa ufanisi kwa maendeleo ya taifa hili? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, anasema nimpatie mchanganuo wa hao watumishi 7,000. Mheshimiwa Tunza nimesema wanaohitajika ni 7,000 ambao tulionao Watumishi walioajiriwa ni 4,751 hawa hata leo hii nikimaliza kujibu maswali haya niko tayari kukupatia hawa 4,751. Kwa hao 7,000 pia niko tayari kukuandalia mchanganuo huo kwa kada zote ambazo zinahitajika na kukupatia ikiwezekana siku ya jumatatu tuwasiliane na nikupatie mchanganuo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, naomba kwanza niseme, si kwamba Mamlaka ya Mapato ina upungufu mkubwa wa watumishi kama alivyosema, upungufu uliopo ni wa asilimia 28 tu siyo upungufu mkubwa. Kwa hiyo kama nilivyosema tunahitaji 7,000 tulionao ni 4,751 na Serikali ya Awamu ya Tano imejitahidi kwa kiwango kikubwa; tangu imeingia madarakani tayari tumeshaajiri Watumishi 692 na kwa mwaka huu tayari kwenye Bajeti yetu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania tutaajiri watumishi 150. Kwa hiyo tunakwenda hatua kwa hatua mpaka mwisho tutakamilisha wote Watumishi 7,000 wanaohitajika ili kuhakikisha Mamlaka ya Mapato Tanzania inafanya kazi zake kwa ufanisi.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa kuwa upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Jiji la Mwanza unahusisha makazi ya watu katika Kata za Shibula na Kahama, na kwa kuwa Mwezi Januari mwaka huu timu ya Mawaziri wanane ilifika katika kata hizo na kuwaahidi kwamba watalipwa fidia zao. Sasa nataka kujua; Serikali inawaambia nini wananchi wa kata hizo kuhusu fidia hizo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kumekuwa na kusuasua katika ukarabati wa Uwanja wa Ndege wa Mkoa wa Mtwara, na taarifa zilizopo ni kwamba kwa sababu hakuna fedha za uhakika. Swali langu; je, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo ili uwanja ule uweze kukarabatiwa kwa kiwango kinachokubalika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwenye eneo hili la Uwanja wa Ndege wa Mwanza wapo wananchi ambao wanadai fidia. Na ni kweli kuna timu ya Mawaziri ambao wanahusika na ulipaji wa fidia hii walikuwa na jukumu la kushughulikia ili wananchi waweze kulipwa mapema. Ninawaambia nini wananchi wa maeneo haya; ninawaambia ule utaratibu unakamilishwa na ni mapema kadri itakavyowezekana watalipwa hizi fidia, kwa hiyo wasubiri tu mambo yanaendelea kukamilishwa.

Mheshimiwa Spika, na niseme na pia Mheshimiwa Mbunge Mabula yuko hapa, anafahamu kwa sababu karibu kila siku anafuatilia juu ya ulipaji wa fidia ya wananchi ambao wengi wako pia kwenye eneo lake. Kwa hiyo wananchi hawa wasiwe na wasiwasi, tunalifuatilia na kulishughulikia suala hili ili waweze kulipwa mapema iwezekanavyo. Lakini pia wakilipwa kuna kazi ambayo nimeitaja itafanyika ili iweze kufanyika, na utaratibu ulivyo ni wananchi walipwe kwanza fidia ili maboresho kadhaa yaweze kuendelea katika uwanja huu.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu Uwanja wa Ndege wa Mtwara, labda nimkumbushie tu Mheshimiwa Mbunge, atakuwa amesahau, ni hivi karibuni tu Mheshimiwa Rais alivyofanya ziara Mtwara alitoa maelekezo na sisi kama Wizara maelekezo yale kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, kuna fedha zilitolewa na kazi inaendelea vizuri katika ujenzi huu wa Uwanja wa Ndege wa Mtwara.

Mheshimiwa Spika, na nikwambie Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu tumejipanga kuhakikisha kila wakati tunaboresha uwanja huu na mwaka wa fedha huu unaokuja Bunge hili, Bunge lako limetupitishia fedha ambazo ni takribani bilioni 4.5, mmetuidhinishia ili sasa hii kazi isilale, kwamba kwa maana ya fedha zilizokuepo katika mwaka huu wa fedha na mwaka ujao tuna fedha za kutosha, hatutasinzia kwenye ujenzi wa uwanja, maboresho yatafanyika tuweze kukamilisha na wananchi waweze kupata huduma ya Uwanja wa Ndege huu wa Mtwara.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri swali hili umepewa siku nyingi na hili swali limeuliza ni lini na ni wapi, umejibu kwa ujumla naomba nifahamu hivyo viwanda vitano vya kuchakata samaki katika ukanda wa Pwani viko maeneo gani, kama na sisi watu wa Mtwara vinatuhusu vipo huko kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bandari umesema utakapokamilika, nataka uwe specific unakamilika lini ili hiyo bandari ipatikane kwa maendeleo ya wavuvi na nchi yetu kwa ujumla, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ni wapi viwanda hivyo vipo; viwanda hivyo katika Mkoa wa Dar es salaam, Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Tanga. Mkoa wa Dar es salaam tunacho kiwanda cha Alfa Cluster, Bahari Food, Pugu Road lakini vilevile Mkoa wa Pwani tunacho Kiwanda cha Abajuko kilichopo pale Vikindu Madafu, Mkuranga na vilevile tunacho kiwanda cha Alfa Cluster, Tanga Jiji ambacho kinafanya kazi ya kuchakata samaki aina ya pweza.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ni lini hasa tutamaliza hii kazi ya upembuzi yakinifu ya ujenzi wa bandari ya uvuvi, tutamaliza. Mkandarasi amepewa muda wa mwaka mmoja kwa hivyo bado yupo ndani ya muda wa kukamilisha kazi yake na hatimaye atuletee ile ripoti ambayo itakuwa na ushauri wa mahala kuzuri zaidi tutakapoweza kuweka bandari yetu lakini na gharama zake za ujenzi wa ile bandari yenyewe. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mikopo hii inahusu watu wenye ulemavu; na swali langu ni kwamba, inapotokea mtu mwenye ulemavu ambaye hawezi kufanya shughuli yoyote, lakini ana mlezi ambaye anamlea. Je, Serikali sasa haioni kuna sababu ya kumkopesha yule mtu ambaye anamlea mtu mwenye ulemavu ili aweze kufanya shughuli itakayomwezesha yule mtu kuweza kumlea vizuri yule mtu mwenye ulemavu? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mikubwa mpaka tulipofikia hapa. Tukumbuke kihistoria kwamba Mfuko huu ulikuwa haufanyi vizuri, lakini kwa taarifa tuliyoitoa mwaka 2020, zaidi ya shilingi bilioni 124 ziliweza kuelekezwa katika makundi haya. Mpaka leo taarifa yetu ya miezi sita mpaka mwezi Desemba, zaidi ya shilingi bilioni 22.45 zimeelekezwa katika makundi hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, nazishukuru Kamati za Bunge hasa Kamati ya TAMISEMIna Kamati ya LAAC katika kutoa ushauri wa uboreshaji wa Kanuni na hasa makundi ya watu wenye ulemavu. Hivi sasa tume-review kanuni zetu za kuhakikisha, hata kama mlemavu ni mmoja, aweze kupata mkopo ambapo hayo yalikuwa ni maelekezo ya Bunge. Hata hivyo, tumeenda katika suala zima la uboreshaji katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, nia yetu ni kwamba Mfuko huu uende kufanya vizuri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dada Malapo, hilo ni jambo ambalo Serikali hivi sasa inalifanyia kazi, lengo likiwa, walemavu waweze kushiriki vizuri katika shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba viwanda hivyo viwili anavyovisema, kimoja kinabangua tani 2,000 badala ya tani 5,000 na kingine hakibangui kabisa, kinafanya kufunga. Swali la kwanza; je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha viwanda hivi vinabangua kwa ule uwezo wake? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; katika Manispaa ya Mtwara Mikindani kuna kiwanda kikubwa cha kubangua korosho kinachomilikiwa na Kampuni ya OLAM. Kiwanda hicho kimefungwa. Kiwanda kile kilikuwa kinaajiri wafanyakazi wasiopungua 6,000 wakiwemo wanawake karibu 5,000. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha wanakaa na mwekezaji yule, kiwanda kile kiweze kufanya kazi ili wanawake wa Jimbo la Mtwara Mjini waweze kupata ajira wajikwamue kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kabisa kwamba, kama nilivyosema katika jibu la msingi, kuna changamoto ya malighali kwa maana ya korosho ambazo zinahitajika katika viwanda vyetu mbalimbali vya kubangua korosho hapa nchini. Hivyo, kutokana na changamoto hiyo, Serikali kupitia Bodi ya Korosho, tumeandaa mwongozo ambao kwanza tunawapa kipaumbele wabanguaji wa korosho hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuanzia msimu wa 2021 mwongozo huo unataka malighafi zinazopatikana katika mnada wa awali kupitia soko la awali la korosho, viwanda vyote vya ndani ambavyo vinabangua korosho, kwanza vipate korosho, vikishajitosheleza ndiyo sasa tunafungua ule mnada wa pili ambao sasa utahusisha wafanyabiashara wote ambao wako katika soko la korosho. Hii itapelekea kuhakikisha kwamba viwanda vyote vinavyobangua korosho vinapata malighafi kulingana na mahitaji yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusu Kiwanda cha OLAM, ni kweli kiwanda hiki ambacho kilikuwa ni sehemu ya uwekezaji katika Manispaa ya Mikindani, changamoto kubwa iliyosababisha kufungwa kiwanda kile ilikuwa ni kutokana na kukosa malighafi ambazo zilitokana na ushindani wa wanunuzi wa korosho katika minada ambayo inafanyika kwenye maeneo hayo. Ndiyo maana tunapeleka mwongozo huu ambao sasa utahakikisha kwamba viwanda vya kubangua korosho vinapata malighafi kwanza, halafu sasa zile zinazobaki ndiyo zitaingizwa kwenye mnada ambao utajumuisha wafanyabiashara wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali tayari imeshaanza mawasiliano na Kampuni ya OLAM ambao waling’oa mitambo ile na kuipeleka nchi jirani Msumbiji ambako wao walikuwa na utaratibu mzuri wa kuhakikisha viwanda vinapata malighafi. Kwa hiyo, sasa tunataka warudi nyumbani kwa sababu nasi tayari tumeshaweka mwongozo huo ambao unawahakikishia malighafi viwanda vyote ambavyo vinabangua korosho hapa nchini. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imejenga mifereji katika baadhi ya maeneo, lakini mfereji wa kutoa maji kutoka Kata ya Shangani, maeneo ya Kiangu kwenda baharini haufanyi kazi vizuri, maji yanajaa sana kwenye majumba ya watu. Sasa swali langu, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kwenda Mtwara kuuona mfereji ule na kufanya utaratibu wa kuhakikisha mfereji ule unatengenezwa kwa kiwango kizuri ili kusudi wananchi wale wasiweze kupata adha hiyo maji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, maeneo mengi ambayo yanajaa maji katika Manispaa ya Mtwara Mikindani ni ambayo Serikali imepima viwanja ikawagawia wananchi, siyo kwamba wamevamia. Katika kujaa maji kule kunasababisha uharibifu na wakati mwingine vifo vya wananchi.

Je, Serikali sasa iko tayari kwenda kukaa na wananchi wale waone wanatatua vipi changamoto hizi kwa sababu kadri miaka inavyokwenda tatizo ni kubwa, linaharibu mali na wakati mwingine kugharimu maisha ya wananchi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza alilokuwa ameliomba, anaomba sisi kama Ofisi ya Rais – TAMISEMI hususani Waziri kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kwenda katika eneo husika kushuhudia anachokieleza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, niko tayari mara baada ya kupitisha bajeti yetu, nitaongozana naye pamoja na Mbunge wa Jimbo husika kuhakikisha tunaipatia ufumbuzi kero hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili ameuliza kama Serikali ipo tayari kukaa na wananchi, nimhakikishie tutakavyokwenda kule tutakaa na wananchi ili tuweze kupata suluhisho la tatizo hilo. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, nataka kujua ni sababu zipi zinazosababisha kusuasua kwa usambazaji wa gesi kwa matumizi ya binadamu katika Mkoa wa Mtwara hususan Manispaa ya Mtwara Mikindani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, sisi watu wa Mtwara kabla hatujapata gesi kwa matumizi yetu, gesi imepelekwa Dar es Salaam na watu wameunganishiwa majumbani. Kwa nini wameanza Dar es Salaam badala ya Mtwara ambako gesi inatoka kwa sababu na sisi pia tuna matumizi nayo? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Tunza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kusema kwamba usambazaji wa gesi katika Mkoa wa Mtwara hausuisui. Tulianza kuzalisha gesi katika Mkoa wetu wa Mtwara mwaka 2015 na mpaka sasa tunatumia umeme wa gesi peke yake kwa Mkoa wa Mtwara, Lindi na mikoa mingine yote ya Kusini. Umeme wote unaotumika kule unatokana na nishati ya gesi. Mpaka kufikia mwezi Julai mwaka huu, tayari nyumba 425 zitakuwa zimeunganishwa na huduma ya gesi majumbani kwa ajili ya matumizi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni la kufurahisha, watumiaji wakubwa sana wa gesi Tanzania wa kwanza ni TANESCO na wa pili ni kiwanda chetu cha Dangote ambacho kiko Mtwara. Kiwanda hicho kinatoa ajira kwa vijana wetu, watu wanalipa kodi na Serikali inapata manufaa makubwa sana. Kwa hiyo, ni mojawapo ya faida kubwa sana ambayo inapatikana kule. Tunazo taasisi kama nne, Magereza, VETA, shule moja ya sekondari na chuo kingine kimoja, zinatumia gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kusema kwa kweli Serikali imejitahidi sana kuhakikisha wananchi wa Mtwara wananufaika na nishati hii. Hata hivyo, kwa sababu nishati ni kwa ajili ya Watanzania wote basi nyingine kidogo inatoka na kwenda kwingineko mpaka hapa Dodoma tutaweza kuifikisha kwa wakati. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, Serikali imejipangaje kutoa elimu ya namna ya kutenga takataka kulingana na makundi yao kwa sababu kuna zile takataka ambazo zinaoza kwenye mazingira, lakini kuna nyingine kama pastiki na hizo chuma chakavu haziwezi kuoza inabidi zifanyiwe recycling zirejeshwe tena naomba kupata mkakati wa Serikali imejipangaje?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la dada yangu Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli changamoto ya takataka ambazo zimechanganyika imekuwa ni jambo kubwa sana hata ukienda katika madampo yetu ya kisasa ambayo yanapaswa kutenganisha zile taka unaona kwamba tumekuwa na changamoto kubwa sana katika kupitia hilo ndiyo maana tarehe 3 Juni tuliwaita hapa Maafisa Mazingira wote kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa na Mikoa yote kwa lengo la kuwapa utaratibu mzima jinsi gani wataweza kutoa elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na ngazi za mikoa kwa ajenda kubwa kwamba mamlaka hizo zikishirikiana na taasisi yetu ya NEMC ziweze kuhakikisha nchi yetu iko salama.

Kwa hiyo Mheshimiwa Tunza Malapo swali lako ni swali muafaka kabisa na hivi sasa Serikali imeshaliwekea maelekezo na mpango huo unaanza mara moja.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa majibu haya Mheshimiwa Waziri ni wazi kwamba suala la ujenzi wa bandari na ununuzi wa meli katika Mkoa wa Mtwara bado. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza; kwa kuwa wavuvi ili waweze kutengeneza vyombo vyao, wanahitaji kununua miti ama mbao kutoka kwa wauza mbao ambao TFS wanatoa kibali kwao. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inawapa vibali wavuvi ili waweze kukata ile miti na kutengeneza vyombo kuepusha gharama inayopatikana kwa kwenda kununua kule kwa wauza mbao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa hakuna uelekeo wa sasa hivi wa kuonekana kutajengwa Bandari ya Uvuvi pamoja na ununuzi wa meli katika Mkoa wa Mtwara, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inawawezesha wavuvi wa Mtwara kupata vyombo vya kisasa vile vya fibbers nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni upatikanaji wa mbao na kwa kuwa vibali vinatoka TFS, Wizara ya Maliasili na Utalii, naomba nichukue rai hii ya Mheshimiwa Mbunge na nataka nimhakikishie yeye na wavuvi wote ya kwamba ndani ya Serikali tutalizungumza jambo hili ili kuweza kuona unafuu wa hao wavuvi ambao wanahitaji mbao 10 hadi 15 waweze kuzipata kwa urahisi kwa ajili ya ku-repair au kutengeneza vyombo vipya kwa kuwa ikizingatiwa wao hawaendi kufanya biashara bali wanakwenda kutengeneza vyombo kwa ajili ya matumizi yao. Kwa hivyo, hili ni jambo jema na nalichukua kwa ajili ya utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala la upatikanaji wa fibbers. Tunaanzisha upya Shirika letu la TAFICO na moja ya hadidu za rejea za kuhakikisha TAFICO mpya iweze kufanya vyema ni kuingia ubia kwa maana ya PPP na Sekta Binafasi na moja ya jambo tutakalokwenda kulikazania kwa huyo mtu atakayekuja kwa ajili ya PPP ya ubia ni kuhakikisha atuoneshe dalili na matumaini ya pamoja na kuvua lakini upatikanaji wa vyombo kuanzia katika ukanda wetu wote wa bahari hata na visiwani pia vilevile kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa samaki kwa kutumia vyombo vipya vya kisasa na hii ni pamoja na Mkoa wa Mtwara.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa Mikoa ambayo inaongoza kwa maambukizi ya malaria ni pamoja na Mkoa wa Mtwara. Nataka kujua mkakati wa Serikali kuhakikisha Mkoa ule unaondoka katika janga hilo la ugonjwa wa malaria. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE
NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mkoa wa Mtwara ni kati ya Mikoa ambayo ina maambukizi makubwa ya malaria, tunalitambua hilo, iko Mikoa ya Lindi, Katavi na mingine mingi. Tunaipa kipaumbele kwa hizi rasilimali tulizonazo hatutazitumia tu hivi randomly. Kwa mfano Arusha, Manyara, pamoja na Moshi wenyewe wameshakwenda kwenye elimination. Kwa hiyo tutaongeza nguvu sana ku- adress haya masuala ya Mikoa ambayo bado maambukizi yapo juu. Tutashirikiana pia na Wizara ya Mazingira kwa sababu suala hili ni mtambuka kuhakikisha kwamba tunaifikia hii Mikoa tushushe kama Manyara, Arusha na Moshi. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, kaa hapo hapo. Sasa hivi kuna mtindo watu wanapita majumbani wanamwaga dawa kwa barua za Halmashauri asilimia kubwa ya dawa hizo ni maji. Hilo nalo mlidhibiti.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE
NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nimepokea na nawatumia salamu huko walipo. Tunaanza kuwafuatilia leo hii tujue walitumwa na nani na kiwango cha ubora wa hizo dawa wanazomwaga. Nasema waache maana Serikali iko kazini. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; miongoni mwa ahadi za uendelezaji wa nishati ya gesi ni pamoja na ujenzi wa kiwanda kikubwa cha mbolea. Naomba nipate ufafanuzi wa Serikali ni lini kiwanda hicho kitajengwa katika mkoa wa Mtwara?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; sisi watu wa Mtwara kila siku tunauliza gesi kwa sababu hatuoni ile michakato ambayo tulikuwa tunaiona pale nyuma. Sasa hivi Mtwara habari ya gesi ni kama haipo, kama imelala. Hata Ripoti ya CAG ukiisoma inaeleza kwamba matumizi ya gesi bado yako chini.

Sasa nataka tu kujua kauli ya Serikali; ni nini hasa inafanya ili sisi watu wa Mtwara turidhike kwamba ile gesi iliyogundulika Mtwara inafanya lile ambalo limekusudiwa na kuinua uchumi wa watu wa Mtwara na Taifa kwa ujumla? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali ilianza majadiliano na wawekezaji wa viwanda vya kutengeneza mbolea kwa kutumia gesi almaarufu kama petrochemicals. Hiyo gesi ndiyo malighafi kubwa katika utengenezaji wa hizo mbolea na vitu vya namna hiyo. Sasa kilichotokea ni kwamba biashara ile ilionekana haikuwa ya kutusaidia na kutufaa kwa kipindi hicho kwa sababu wakati duniani wanataka kununua kwa dola tatu sisi wa kwetu walikuwa ana bei ya chini kabisa ambayo ilionekana haitakuwa faida kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa tumefungua upya milango ya majadiliano na wawekezaji mbalimbali wanaotaka kuwekeza katika viwanda kama hivyo akiwemo mwekezaji mkubwa wa Dangote naye ameonesha nia na bado tunaendelea kupokea maombi na majadiliano mbalimbali yanafanyika kuhakikisha kwamba sasa tunaweza kutumia gesi kutengeneza viwanda vya malighafi mbalimbali kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunakoelekea ni kuzuri na viwanda vya petrochemicals na vingine vitakuja. Gesi tutaitoa huko iliko na kuitumia kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili; ni kweli kwamba kwa muda mrefu kidogo pameonekana kama pamelala kwamba hakuna kilichokuwa kinaendelea. Kimsingi kilichokuwa kinaendelea ni kikubwa kuzidi kilichokuwa kinaonekana. Tunayo mikataba inayoitwa Production Sharing Agreement (PSA) ni mikataba ambayo inaingiwa kati ya Serikali na wale wawekezaji wanaokuja kuwekeza katika maeneo yetu ya gesi. Tukikubaliana tutazalishaje, tutagawana vipi na tutatumia vipi.

Mheshimiwa Spika, sasa majadiliano hayo yamechukua muda mrefu na marekebisho na mapitio ya mikataba hiyo imechukua muda mrefu, lakini sasa yamekamilika na tayari Serikali imetoa maelekezo na sasa kinachofanyika ile Kamati ya Serikali ya ku-negotiate mikataba imerudi tena kazini na tunatarajia mwezi wa 10 itakuwa imekamilisha kazi yake ya ku-negotiate sasa mikataba ya matumizi na unufaikaji wa gesi na tunatarajia kuanzia mwezi wa 11 basi mambo yataanza kuwa vizuri. Gesi hii tunayoitoa na kuitumia sasa itaongezeka zaidi kwa ajili ya manufaa ya nchi kwa ujumla. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la x-ray katika hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Ligula mimi niliuliza hilo swali Bunge lililopita Naibu Waziri wakati ule Mheshimiwa Ndugulile aliniambie x-ray machine ya Mkoa wa Mtwara ipo bandarini, leo majibu ya Naibu Waziri anaongea as if hakuja kitu kabisa. Mimi nataka tu kujua ile x-ray yetu ambayo tuliambiwa ipo bandarini ime-evaporate au vipi? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze dada yangu mpambanaji kwa swali lake zuri ambalo linahusu wananchi; moja ni kwamba anasema kwamba x-ray hiyo ilikuwa ipo bandarini na mpaka sasa haijafika kwenye eneo husika. Nikuombe dada yangu tukimaliza maswali hapa twende mimi na wewe tukakae pale tufuatilie hiyo x-ray na tuweke utaratibu iweze kufika mapema inapotakiwa, ahsante sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba tu Serikali inieleze, inakuwa wapi mpaka matatizo haya yanatokea? Ukizingatia kwamba watu wengi wanaoweka na kukopa kwenye hizo taasisi ni watu wa kipato cha chini; Serikali inakuwepo inaona jambo linaendelea mpaka linakua, wanakuja kunyang’anya ama kuchukua, watu wanaathirika. Kumbuka mambo ya DECI, ilikuwa hivi hivi. Leo PRIDE iko hivi hivi. Nataka nijue, Serikali inakuwa wapi mpaka inaacha mambo haya yanafikia hapo wananchi wanaathirika ambapo wengi wao ni wakipato cha chini? Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kazi ya Serikali kutoa miongozo na kusimamia hizi taasisi. Kwa upande mmoja Serikali ni pamoja na wananchi inapofika masuala ya kifedha kwa sababu taasisi zote za kifedha zinakuwa na mikutano yao ya kila mwaka, lakini mara nyingi sana wananchi wetu wakishaweka fedha kwenye maeneo haya ya kibenki, hawafuatilii sana mienendo ya kifedha kwenye maeneo walikoweka. Wakati Serikali inafanya yale mambo ya kiutawala, ni wajibu wao pia kuangalia mwenendo wa taasisi yao ambako wameingia mkataba na taasisi husika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, rai yangu, kwanza wananchi watumie taasisi za kifedha ambazo hazina mashaka mashaka. Tuna mabenki yanaendelea kuenea katika maeneo mengi, watumie mabenki ambayo yako accredited na Serikali, wasitumie taasisi zile ambazo zina mashaka mashaka, lakini hata taasisi zile ambazo ziko accredited kama ambavyo masharti ya kifedha yanasema, wanapokuwa na mikutano ya mwaka ya taasisi hizo, wachukulie umuhimu kufuatilia mienendo ya taasisi hizo ambazo wameingia mkataba nazo.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli Hospitali hiyo ya kanda imeanza kutoa huduma, lakini lengo la Hospitali ya Kanda ni kutoa huduma za rufaa. Huduma hizo hazijaanza kwa sababu hakuna vifaa na hakuna madaktari bingwa. Sasa swali langu: Ni lini vifaa na madaktari bingwa wataletwa katika hospitali hiyo kwa sababu hiyo ndiyo shida yetu sisi watu wa kusini hususan Mkoa wa Mtwara? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Ukiangalia mazingira ya nje ya hospitali ile, bado yapo shaghalabaghala, ni lini yatawekwa katika mandhari ambayo inaendana na mandhari ya hospitali? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL): Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri sana; na kweli mawazo mazuri aliyoyatoa ndiyo mwelekeo wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwanza hospitali hiyo imeanza na ni kweli bado watumishi hawajafikia idadi aliyoisema. Tumegawa uanziswaji wa hiyo hospitali. Ukiangalia hospitali yenyewe sasa ina umri wa mwezi mmoja na siku nane, lakini tumegawa uanzishwaji wake kwa phase tatu, maana yake tumeanza phase ya pili ambayo sasa wanaenda kuwekwa watumishi.

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imetenga shilingi bilioni saba kwa ajili ya hospotali hiyo na tayari shilingi bilioni tatu zimeingia kwa ajili ya kununua CT-Scan na MRA. Kuna specialist mmoja na mwezi ujao wanapelekwa 4 ili wafikie 5. Mpaka mwezi wa Pili ambapo tutaenda kwenye Phase ya tatu ya uanzishwaji wa hospitali, tutakuwa na watumishi 217. Kwa hiyo, Mheshimiwa ukitembelea mwazi wa tatu utakuta imeanza kama ulivyotaka wewe.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kuhusu mazingira ya Hospitali. Kweli nimeyaona na mimi wakati jiwe la msingi linawekwa, bado mazingira yaliyozunguka siyo safi. Wakati tunaendela kwenye phase hizi, tunaendelea kuhakikisha vile vile na usafi unafanywa.

Mheshimiwa Spika, OC imetengewa shilingi milioni 600. Kwa hiyo, watatumia kwa ajili ya kuhakikisha mambo mengine yanakuwa sawa na kufikia lengo ambalo Wana- Mtwara wangetegemea kuona.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa mujibu wa muuliza swali alitaka kujua ni lini Mheshimiwa Waziri hajajibu. Sasa na naendelea kuuliza ni lindi stendi hiyo itaboreshwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, tatito lililopo katika stendi hiyo ya Bweri Musoma ni sawa kabisa na tatizo ambalo lipo katika stendi ya Mkoa katika Jimbo la Mtwara Mjini, stendi ipo eneo linaitwa Mkanaleli. Stendi ile ni mbaya sasa hivi mvua zinaponyesha maji yanatuama.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha inaboresha stendi ile iendane na viwango kama zilivyo stendi katika mikoa mingine na majimbo mengine?

Mheshimiwa Mwenyekti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu ya msingi nimesema kwamba Serikali tayari imeanza mazungumzo na Benki ya BADEA ili kupata ufadhili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi ya Bweri katika Manispaa ya Musoma Mjini, na ujenzi huo utaanza wakati wowote mara fedha hizo zitakapopatikana.

Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wakati wowote fedha hizo zikipatikana kazi ya ujenzi wa stendi ile utaanza mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kuhusiana na stendi ya Mkanaleli naomba nimpe wito Mheshimiwa Mbunge lakini pia niwaelekeze Mamlaka za Serikali za Mitaa kwamba, miundombinu hii yote stendi lakini na miundombinu mingine ipo chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa, wanawajibika kuhakikisha wanatenga bajeti kujenga au kukarabati stendi hizo lakini kama uwezo wa kibajeti hautoshelezi kutenga bajeti hizo basi wanaelekezwa kuandaa maandiko maalum kwa maana ya maandiko ya kimkakati ili kuweza kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa stendi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe wito kwa halmashauri hiyo kuhakikisha wanafanya tathmini mara moja ya uhitaji wa ujenzi wa stendi hiyo na kuona uwezo wao wa kuijenga lakini kuomba miradi ya kimkakati ili Serikali iweze kusaidia kujenga stendi hizo. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru, nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, matatizo ya Wakurugenzi katika halmashauri mbalimbali yanakuwepo na Madiwani wanayaona na saa nyingine wanayaripoti lakini hayafanyiwi kazi mpaka mwenye Mamlaka labda Mheshimiwa Rais apite ndiyo unakuta hatua zinachukuliwa. Mheshimiwa Waziri haoni sasa ni wakati muafaka wa kuhakikisha au kutoa maelekezo kwa wale wenye dhamana wanapoletewa malalamiko kutoka kwa Watumishi au Madiwani wayafanyie kazi na siyo kusubiria mpaka Mheshimiwa Rais apite ndiyo aende kutengua utenguzi wakati matatizo yalikuwa yanaonekana siku nyingi na Mkurugenzi pale ameleta athari kubwa katika ujenzi wa Taifa?Ninakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa taratibu za utumishi wa umma, mamlaka za nidhamu za wakurugenzi ziko katika ngazi tofauti, kama nilivyotangulia kusema, ngazi ya Katibu Mkuu Kiongozi, lakini pia Waziri mwenye dhamana. Lakini Waheshimiwa Madiwani wana nafasi na mamlaka ya kutoa taarifa ya changamoto ambazo mkurugenzi anapitia katika utekelezaji wa majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, hatua zimekuwa zinachukuliwa kwa wakati, lakini kuchukua hatua ni mchakato kwa sababu, kuna taratibu za uchunguzi, lakini pia kujiridhisha na yale mapungufu yanayoripotiwa kwa mkurugenzi husika, ili kuweza kutenda haki. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba, Serikali itaendelea kufuata taratibu hizo, kufanya uchunguzi kwa wakati, lakini pia, kuchukua hatua ili kutenda haki. Na kuhakikisha kwamba, halmashauri zetu zinakwenda vizuri. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, nataka tu kujua Serikali ilipofanya tafiti imegundua ni kwanini wafanyabiashara wengi hasa wadogo wadogo wanafunga biashara zao hivyo kupelekea hali ya uchumi kudolora hususan Mkoani kwetu Mtwara?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nataka tu kujua mkakati wa Serikali ukoje kuhakikisha unawaunganisha wananchi wa mkoa wa Mtwara na fursa ya masoko katika nchi ya Comoro?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, moja ya mikakati tunayoifanya ni kuhakikisha tunafanya tafiti mbalimbali. Moja kwa kuwashirikisha taasisi za umma lakini pia na wadau wa maendeleo ambao wanafanya tafiti hizo kuhusiana na hali ya uchumi lakini pia na namna ya kufanya biashara nchini.

Mheshimiwa Spika, moja ya matokeo ambayo yanaonesha pamoja na kwamba kuna udolora wa wafanyabiashara wadogo lakini ni changamoto za maeneo. Ndiyo maana Serikali imekuja na mpango wa kuwapanga katika maeneo mahususi ili wawe na maeneo ambayo ni mazuri na rafiki kwa wafanyabiashara wadogo wadogo ambao mara nyingine wakikaa maeneo ambayo si rafiki kunakuwa na ile changamoto zak ukimbizwa na baadhi ya mgambo na taasisi zingine ambazo wafanyabiashara wadogo wanakuwa wamevamia na kufanya biashara zao katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, ni kweli tunaendelea kutafuta, moja ya changamoto yao ya mitaji ambayo tunaifanyia kazi ili wafanyabiashara wadogo wadogo waweze kupata mitaji kwa njia rahisi. Lakini zaidi pia tutaendelea kuwatafutia maeneo ya kufanyia biashara katika Mkoa wa Mtwara kama ulivyosema lakini pia na maeneo mengine nchini, ili wafanyabiashara wadogo kwanza wapate mitaji lakini pili wawe na maeneo mahususi ya kufanya biashara bila kusumbuliwa.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Lindi Sokoine ni sawa kabisa na tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara Ligula, kukosekana kwa Daktari wa magonjwa ya ndani pamoja na mifupa. Je, Serikali ina kauli gani kutuletea, ingawa tunajua tunayo hospitali ya Rufaa lakini hii ni kuhusu ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nimemwelewa Mheshimiwa kwa sababu sijaiangalia vizuri kama ya Mtwara lakini kwa kweli wana bahati moja kwamba, wana hospitali ya Mkoa ambayo ina baadhi ya specialists lakini haijafika hata kilometa moja kutoka Hospitali ya Mkoa kuna Hospitali ya Kanda, ambayo nayo ina Mabingwa. Kwa hiyo, mimi na wewe tutakuja tuangalie specifically tatizo ni nini ili tushirikiane na Mheshimiwa Waziri tuone tunafanya nini.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Lindi Sokoine ni sawa kabisa na tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara Ligula, kukosekana kwa Daktari wa magonjwa ya ndani pamoja na mifupa. Je, Serikali ina kauli gani kutuletea, ingawa tunajua tunayo hospitali ya Rufaa lakini hii ni kuhusu ya Mkoa?
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nimesimama ili kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali kwa sasa ina mpango maalum wa kusomesha Madaktari Bingwa na Madaktari Bingwa Bobezi ambapo katika Mwaka huu wa Fedha wa 2022/2023 tutasomesha Madaktari Bingwa na Bobezi 139. Madaktari Bingwa na Wabobezi 136 tutawasomesha nje ya nchi. Tumeamua kuwasomesha kwa utaratibu wa set badala ya kupeleka Daktari Bingwa Mmoja wa magonjwa ya ndani inabidi awe na Muuguzi Bingwa wa masuala ya usingizi, kuwepo na mtoa huduma Bingwa wa radiology, kwa hiyo ndiyo jambo ambalo tunaenda nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tuna Madaktari Bingwa 457 tunawasomesha katika pair moja moja. Kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, kwanza tutafanya assessment, tunafahamu kuna baadhi ya hospitali za Rufaa za Mikoa zinazo idadi kubwa ya Madaktari Bingwa kuliko hospitali za pembezoni. Mheshimiwa Waziri wa Utumishi, ameshanipa kibali kama wamezidi niwahamishe ili kuwapeleka ambako kuna shida wakati tukiendelea kusubiri hawa ambao tunawasomesha.

Mheshimiwa Spika, tunatambua ni changamoto kubwa lakini ndani ya miaka miwili itakuwa ni historia chini ya mpango wa Samia Suluhu Health Super Specialization Program. Ahsante sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.

Kwa kuwa vitendo vya ukatili vimezidi kuongezeka kila siku tunasikia matukio mbalimbali, na kwa kuwa adhabu mbalimbali zinatolewa lakini vitendo vinazidi kuongezeka.

Je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka wa ku-review hizi adhabu ili ziwe kali zaidi watu wasiendelee kufanya hivi vitendo vya ukatili? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametoa wazo zuri nadhani ni jambo la kulichukua na kulitafakari na kulifanyia kazi. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza; ili zao hili liweze kufufuka na kuleta tija sio kupeleka mbegu bora tu ni pamoja na kutafuta masoko mazuri nay a uhakika ili wakulima waweze kuuza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha masoko ya uhakika yanapatikana?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; sisi Mkoa wa Mtwara muhogo ukilimwa unastawi kweli kweli lakini tunashindwa kulima kwa sababu hakuna kiwanda cha kuongeza thamani ya zao la muhogo. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inajenga kiwanda yenyewe ama kushirikiana na sekta binafsi ili kuongeza thamani ya zao la muhogo? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika swali la kwanza la kuhusu masoko hivi sasa Wizara tumeendelea kuimarisha huduma za masoko kwa kuhakikisha kwamba mazao yetu mengi tunayatafutia masoko, ili wakulima wetu wakilima kwa tija mwisho wa siku mazao yao yaweze kupata masoko ya uhakika. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba moja kati ya mkakati tulionao hivi sasa ni kufanya muhogo kama sehemu ya malighafi kuu katika viwanda vyetu ambavyo tumeanza mazungumzo nao kwa ajili ya kutengeneza wanga ambao hivi sasa tunaagiza karibuni tani 8,000 kwa mwaka. Kwa hiyo, tumeanza mazungumzo na viwanda vilivyoko hapa nchini kwa ajili ya kufanya muhogo kama malighafi ya utengenezaji wa wanga. Zoezi hilo linakwenda vizuri na mwitikio umekuwa mkubwa na ndio maana sasa tumeendelea kuhamasisha wakulima wengi zaidi kulima muhogo.

Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusu viwanda. Ni kweli mwisho wa siku kama Wizara katika mkakati wetu ni kuhakikisha kwamba tunaongeza thamani ya mazao yetu na kwa upande wa muhogo viko viwanda ambavyo mwanzoni vilionesha nia ya kuanza kufungua katika upande wa kule Kusini. Kwenye Kijiji cha Malamba katika Jimbo la Mtama ipo kampuni ambayo ilifungua kiwanda, Kampuni ya Cassava Starch of Tanzania Corporation bahati mbaya sana walipata changamoto ya mtaji na hivi sasa wana administration order ya Mahakama ya Biashara Management wameamua kukichukua kiwanda kile na wanatafuta wawekezaji. Wameshakuja wawekezaji kutoka Japan na maeneo mengine na sisi kama Wizara tunaendelea kuwasaidia kutafuta wawekezaji ili kiwanda kile kifufuliwe na kiwe sehemu ya uchakataji wa muhogo ya wakulima wa Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Lindi na Mikoa yote ya Kusini. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Walimu wengi wanakosa viti na meza nzuri za kukaa na kuweza kufanya kazi zao vizuri. je, Serikali inalijua hilo na ina mkakati gani wa kulitatua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mtwara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunatambua changamoto hizo katika baadhi ya shule na tunazifanyia kazi. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kama chujio limekamilika kujengwa, kwanini maji yanatoka machafu na wakati mwingine wananchi wanashindwa kuyatumia?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Mkataba wa uboreshaji wa miiundombinu ya maji katika Manispaa ya Mtwara Mikindani wenye thamani ya Shilingi bilioni 19 ulisainiwa mbele ya Mheshimiwa Waziri. Nataka kujua utekelezaji wake umefikia hatua gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la maji kutoka machafu baada ya ukamilishaji wa chujio ni suala la kiufundi. Ni sehemu chache ambapo mabomba ni chakavu wakati fulani bado yanaleta udongo kwa ndani lakini tayari watendaji wetu wanalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mkataba kusainiwa mbele ya Mheshimiwa Waziri uko sahihi, tayari Shilingi bilioni 19 zimetengwa, Mkandarasi ameshapatikana, yuko kwenye mobilization, anafanya uandaaji wa site na hivi punde atalipwa advance payment ili kazi zianze.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama ilivyo ugonjwa wa fistula pia maambukizi ya virusi vya UKIMWI bado ni janga kwenye nchi yetu, lakini inaonekana kama Serikali imelegalega katika kutoa elimu. Mimi nataka kujua;

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuendelea kutoa elimu ya kujikinga na virusi vya UKIMWI kwa wananchi wetu wa Tanzania?
NAIBI WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani anachosema, Serikali haijalegalega lakini ni strategy tu zimebadilika kwa ku-approach kulingana na hatua ambazo tumefikia. Kwa sababu ukiangalia hali ya maambukizi sasa hivi imeshuka sana na hali ya maambukizi ni makubwa kwa makundi maaulum na nguvu zinaelekezwa kwenye makundi maalum kuhakikisha hali hiyo inadhibitiwa.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kama ilivyo kwa Kiwanda cha Mbolea Kilwa, ni sawa kabisa na ilivyo na uhitaji wa Kiwanda cha Mbolea Mtwara, hususan Jimbo la Mtwara Mjini kwa sababu malighafi ipo. Sasa tu nataka kujua, ni lini Serikali itajenga kiwanda hicho kwa sababu kitaongeza ajira na wakati huo huo itawezesha nchi kupata mbolea kwa ajili ya kilimo?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, Serikali ina nia njema kuhakikisha tunavutia wawekezaji wengi kuwekeza katika viwanda vingi ikiwemo viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Spika, pia hili la Mtwara nalo tunalichukulia kwa umuhimu wake kwamba tutaendelea kutafuta wawekezaji zaidi ili weweze kuwekeza Mtwara na maeneo mengine ambayo yana malighafi kwa ajili ya kuzalisha mbolea. Nakushukuru.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nataka tu kujua wanasema kubaini maeneo mapya ya uwekezaji kwani yale ya zamani Mheshimiwa Waziri mmeyaendeleza? Hilo swali langu la kwanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule kwetu Mtwara hususan wilaya ya Mtwara ambayo inahusisha Jimbo la Mtwara mjini na Mtwara Vijijini kuna fukwe nzuri sana ambayo ikiendelezwa itavutia utalii na hivyo kusababisha shughuli za maendeleo pale Mtwara zipatikane sasa swali langu. Serikali imejipanga vipi kuhakikisha wanatangaza fukwe zile zinaendelezwa ili watalii waje? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Tunza kwa kuliona hili na mimi niseme tu kwamba haya maeneo ambayo ni maeneo ya fukwe kwa asilimia kubwa yanamilikiwa na Serikali za Mitaa lakini pia na wananchi binafsi. Kwa hiyo sisi tumekuwa tukitafuta wawekezaji lakini baada ya kutafuta wawekezaji tunawapeleka katika wamiliki ambao wanamiliki haya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo baada ya Royal Tour ambayo Mheshimiwa Rais, tunamshukuru sana, ameizindua na pia kutafuta wawekezaji tumetengeneza namna na mbinu bora ya kuwakutanisha sasa hawa wamiliki wa maeneo haya na kuyaweka wazi na kuyasajili ili sasa kuwepo na uwezekano ukipata mwekezaji basi unamuonyesha tu kwamba nenda hapa.

Kwa hiyo nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi Serikali inayashughulikia kwa ukaribu na hivi punde tutaanza kuwaona wawekezaji wengi wanaenda kwenye maeneo haya na tutahakikisha wanayapata kwa sababu tayari tumeshaanza kuyasajili na wamilki wameshakuwa wazi na wameshaanza kuiona Serikali na tayari tuna mpango mzuri ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza; miongoni mwa watu wanaolima chumvi kwa wingi ni wakazi wa Mkoa wa Mtwara, changamoto kubwa wanayoipata ni soko la uhakika. Nataka kujua mkakati wa Serikali ni upi kuhakikisha wakulima wale wa chumvi wanapato soko la uhakika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ili kuchochea uchumi wa bluu; uwepo wa dhana bora za uvuvi ikiwemo meli ya uvuvi ya kisasa ni jambo la muhimu. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuleta meli ya kisasa ya uvuvi katika Bahari ya Hindi iliyopo Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA:
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli moja ya changamoto kubwa tuliyonayo kwa wazalishaji wa chumvi hasa wadogo ni changamoto ya soko la uhakika kwa chumvi yao na hasa ambayo ni malighafi kwa maana ya kuwa siyo finished product.

Mheshimiwa Spika, moja ya mikakati ya Serikali tumeshaanza kutekeleza na kuzuia uingizaji wa malighafichumvi au chumvi ambayo inatumika kuzalisha chumvi ya kula kutoka nje. Hili tumeshalisema na tunaamini viwanda vya ndani vinavyozalisha chumvi vitatumia malighafi zilizopo kwa maana ya chumvi inayozalishwa na wakulima wadogo wadogo wakiwemo wa Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Spika, zaidi tunahamasisha katika masoko ya kikanda kwa maana ya Afrika Mashariki na SADC ili tuone nchi ambazo zinakosa au hazina malighafi ya chumvi zinatumia malighafi ya chumvi yetu ikiwemo inayotoka katika Mkoa wa Mtwara ambao tunaamini itakuwa ni chumvi ambayo inapelekwa kwenye masoko hayo ili waweze kunufaika zaidi na uzalishaji wa chumvi katika maeneo haya ya Mtwara.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa meli ya kisasa ya uvuvi kama nilivyosema Serikali tunaedelea kuhamasisha uwekezaji katika maeneo yote ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha uchumi wa bluu ambayo nayo inahusisha kuwa na meli za kisasa ambazo zingeweza kusaidia kuwa na uvuvi wa kisasa zaidi wenye tija. Serikali pia kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea na mikakati mbalimbali ambayo mojawapo ni kuona namna gani ya kutafuta wawekezaji wengi ambao wanaweza kuvua kwa tija katika bahari yetu.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara hiyo ndiyo inaelekea Makao Makuu ya Halmashauri. Kwa kujenga kilometa mbili kwa mwaka barabara ya kilometa 79; je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi kabisa wa kuimaliza barabara hii kwa wakati kwa kuzingatia umuhimu wake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Nataka Serikali inieleze kwa dhati ya moyo kabisa, inamaliza lini Barabara ya kutoka Mtwara Mjini kupita Tandahimba – Newala mpaka Masasi ile ya kilometa 210? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, Mtwara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii kweli ni ndefu na inaenda kwenye Makao Makuu ya Wilaya. Ndiyo maana tumeshaifanyia usanifu, lakini kadiri fedha inavyopatikana tumeona tuanze kuijenga wakati tunatafuta fedha ya kuijenga yote kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, dhamira ipo ndiyo maana tumeanza.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, barabara ya kilometa 210 ya kutoka Mtwara – Mnivata – Newala hadi Masasi, Serikali imeshaanza kuijenga; kilometa 50 kutoka Mtwara hadi Mnivata, na sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya kuanza kuijenga barabara yote kuanzia Mnivata hadi Masasi. Tumegawa lots mbili, kwa wahisani ya wenzetu wa African Development Bank ambao wanafadhili hiyo barabara, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, swali langu, nataka kujua ni lini Serikali itaanza ujenzi wa shule ya mkoa ya mfano ya wasichana katika Mkoa wa Mtwara kama ilivyojenga kwenye mikoa mingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kujenga shule hizi katika kila mkoa na tayari bilioni 30 ilishatoka kwa ajili kujenga shule kumi kwenye mikoa kumi ambao kila mkoa ilipata bilioni tatu. Tunaenda sasa kwenye hatua ya pili ambapo mikoa mitano itapokea hizi bilioni tatu pia kujenga na awamu ya tatu pia tutamalizia hizo shule nyingine na tutahakikisha Mkoa wa Mtwara pia nao unapata shule hii kwa wakati.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika nakushukuru. Kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hii ya uchumi, ni nini hasa mkakati wa Serikali kuhakikisha inajenga barabara hii kwa haraka?

Swali langu la pili, Jimbo la Mtwara Mjini lina changamoto kubwa sana ya barabara; je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuliangalia jimbo hili kwa jicho la tatu ili iweze kulijengea barabara nyingi za lami?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunatambua umuhimu wa barabara hii kama Serikali na ndiyo maana tumeshafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na tunahakikisha ya kwamba barabara hii inapitika kila mwaka. Katika mwaka wa fedha ujao imetengewa takribani shilingi milioni 188.435 na katika mwaka ujao pia tutafanya usanifu wa kina ili iwe maandalizi katika kujenga katika kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, barabara katika Mkoa wa Mtwara hususan Mtwara Vijijini na Mjini, Serikali inatambua umuhimu wa barabara kuboreshwa katika Mkoa huo. Ndiyo maana hivi sasa kuna miradi ile ya EPC + Financing, kuna barabara ambazo pia ziko katika Mkoa wa Mtwara na ambazo hivi karibuni tutaenda kusaini mkataba kabla ya mwezi wa sita mwaka huu, 2023, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Reli ya Kutoka Mtwara mpaka Mbamba Bay ni miongoni mwa miradi midogo iliyopo katika Mradi huu mkubwa wa Mtwara Corridor. Serikali imesema itatekeleza mradi huu kwa ubia. Mimi nataka kujua kwa nini Serikali isitekeleze mradi huu yenyewe ikizingatia umuhimu wake kuliko kusubiria ubia ambao hauna uhakika utapatikana lini?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, mwaka 2004 Lilongwe – Malawi kulisainiwa mkataba wa utekelezaji wa Mradi huu wa Mtwara Corridor na Tanzania inatakiwa iitishe Mkutano ili kutathmini utekelezaji wa mradi huu umefikia hatua gani? Mpaka leo Tanzania haijaitisha: Nataka kujua, ni lini Serikali ya Tanzania itaitisha mkutano huo wa nchi nne; Msumbiji, Malawi, Zambia na Tanzania yenyewe ili kutathmini mradi huu umefikia hatua gani kwa sababu ni mradi muhimu sana katika mikoa ya kusini?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya uamuzi wa kuzishirikisha sekta binafsi ili kuongeza tija. Pia, kwa sababu Serikali ina commitment nyingi, inaweza ikachelewa kupata fedha kwa ajili ya huu mradi. Hata hivyo, kuna makampuni zaidi ya manne kutoka China, South Africa, Australia pamoja na Marekani, ambao wameonesha nia ya kuwekeza katika mradi huu wa ubia, ukizingatia kwamba eneo hili tayari ni potential kubwa. Uwepo wa makaa ya mawe pamoja na chuma unasababisha wawekezaji hawa waje. kwa sababu tayari mzigo upo metric ton zaidi ya milioni 428 ambapo tunaweza tukachimba zaidi ya miaka 100. Kwa hiyo, sekta binafsi tayari imeonesha utayari huo. Kwa hiyo, tutaendelea kuwa-engage ili mradi huu uweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka kujua ni lini sasa Mkutano wa Wakuu wa Nchi utaitishwa. Tarehe 15 ya Mwezi wa Sita kutakuwa na mkutano wa wadau wote wa sekta na Wizara ya Madini, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Uchukuzi, wadau kutoka sekta binafsi pamoja na taasisi zote za Serikali hususani TRA, MSCL, TPA, RAS Mtwara, RAS Lindi na Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara na Lindi mnakaribishwa kwa ajili ya kujadili jambo hili kama maandalizi ya kuzi–engage nchi zingine za Msumbiji pamoja na Malawi, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kule kwetu Mtwara wananchi wamehamasika kufuga majongoo Bahari kwenye vizimba, lakini tatizo kubwa ni vifaranga. Nataka kujua ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha wafugaji wale wanapata vifaranga kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, namshukuru sana Mheshimiwa
Mbunge, amezungumzia suala la majongoo bahari ambayo ni moja ya bidhaa kubwa ambayo sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tunaitangaza. Niwaondoe shaka wananchi wa ukanda ule. Sasa hivi moja ya mkakati wa Serikali, tunaanzisha kituo cha kuzalisha vifaranga katika Mkoa wa Mtwara ili kuhakikisha kwamba uzalishaji wake unakuwa wa haraka na kwa ukaribu zaidi. Kwa hiyo, huo ndiyo mkakati wa sasa na tunalifanya hilo kwa haraka iwezekanavyo.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tatizo linalowakumba wavuvi wetu nchini ni kukosa zana bora za uvuvi. Serikali katika bajeti yake ilisema itanunua meli za uvuvi ili igawe, ipeleke katika sehemu mbalimbali. Nataka kujua, mkakati huo umefikia hatua gani? Kwa sababu Mtwara kule sisi hatujapata hiyo meli. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika bajeti ilielezwa, lakini pia tumeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuwasiliana kwanza kwenye masuala ya fedha, kuhakikisha tunapata fedha na kutekeleza bajeti kwa kadri ilivyokuwa imepangwa kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, yale yote ambayo tuliyapitisha katika bajeti, tupo kwenye hatua za utekelezaji na tutahakikisha kwamba tunayatekeleza kama ambavyo tumekuwa na matamanio, likiwemo hilo la kuweza kununua meli na kuboresha katika sekta hiyo ya uvuvi kwa kuleta mitambo ya kisasa na pia kutumia teknolojia ya kisasa, ahsante. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Miundombinu ya soko la samaki katika Manispaa ya Mtwara Mikindani ni mibovu na mibaya hasa sehemu ya jiko pamoja na ofisi. Nini mkakati wa Serikali kuboresha miuondombinu hiyo? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, soko la Mikindani ni kama masoko mengine ambayo nimeshatoa maelekezo, kwamba tutatuma wataalam kuja kuangalia upungufu uko wapi, halafu baada ya kuyajua huo upungufu, Serikali iko tayari kuanza kufanya marekebisho ya maeneo hayo. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, je, ni lini Serikali itajenga upya ama kukarabati jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Likombe kilichopo Manispaa ya Mtwara Mikindani? Jengo hilo limechakaa, na la zamani, halikidhi mahitaji ya sasa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kutumia fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI tathmini ya gharama zinazohitajika kwenye kufanya ukarabati lakini pia kama ni kufanya ujenzi mpya, ili tuweze kuona kama gharama hiyo ipo ndani ya uwezo wa mapato ya ndani ya Halmashauri. Tutatoa maelekezo ili waanze kutenga fedha mwaka wa fedha 2024/2025. Kama ipo nje ya uwezo wao, Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa maana ya Serikali Kuu, itaangalia namna ya kuwaunga mkono kupitia fedha ya Serikali Kuu.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama ilivyo Mkoa wa Songwe pia katika Mkoa wa Mtwara kuna vijiji 102 bado havijapatiwa umeme. Nataka kujua Serikali ni lini itavipatia vijiji hivyo umeme?
Swali la pili, kwa kuwa umesema mnafanya mchakato wa kutambua Kata ambazo zina hadhi ya Miji lakini ni Vijiji. Nataka kujua ni lini mchakato huo utakamilika ili watu wapate huduma kwa sababu hata katika Jimbo la Mtwara Mjini kuna baadhi ya Kata mfano Kata ya Naliendele, Kata ya Jangwani na zingine zinaonekana ziko Mjini lakini maisha ya watu wake ni kama wako vijijini, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, alivyosema kama ilivyosomwa lakini na Mtwara pia tunao Wakandarasi wawili, wanafanya kazi katika Mkoa wetu wa Mtwara na juzi tulikaa kikao na Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara tukajadiliana kwa upana namna ya kumaliza haraka kazi hizo, tunaamini kwa mkakati tuliouweka kabla ya Desemba mwaka huu kazi yetu ya kupeleka umeme katika vijiji vyote vya Mkoa wa Mtwara itakuwa imekamilika na hilo tunauhakika nalo na tunawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwa kutupitishia bajeti juzi tutaendelea kusimamiana na wenzetu ili kazi hii iweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni lini tutamaliza kazi hii, tunatamani hata tuimalize leo lakini kwa sababu ya kutaka kufanya ushirikishwaji mkubwa na kubaini changamoto za maeneo mbalimbali tunaomba mtuongezee muda kidogo halafu baadae tutakuja kusema ni lini tutamaliza ili tuweze kukamilisha hii kazi kwa Pamoja, tusingependa kuikimbiza harafu ikawa kama ya awali ambayo haikuleta majibu tuliyokuwa tunayatarajia kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza nataka kujua mkakati wa Serikali wa kuhakikisha unawapatia mbegu bora kwa ruzuku wakulima wa mazao haya mengine.

Swali langu la pili, nataka kujua kuna changamoto kubwa sana ya masoko hasa ya zao la muhogo pamoja na mbaazi wakulima wanalima lakini wanakosa masoko ya uhakika. Nataka kujua mkakati wa Serikali kuhakikisha masoko ya mazao haya yanapatikana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upatikanaji wa mbegu kwa ajili ya wakulima kwa mfumo wa ruzuku. Sisi kama Serikali tuko tayari kuhakikisha kwamba tunaongeza uzalishaji wa mazao haya na pindi pale mahitaji yakiainishwa kupitia TARI na ASA tupo tayari kuwapatia wakulima mbegu hizi katika mfumo wa ruzuku ili waweze kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu masoko ya uhakika, nikianza na mbaazi, kwenye mbaazi tayari tumeshaingia makubaliano ambayo bado tuko katika hatua za mwisho na Serikali ya India ya kuchukua zaidi ya tani 150,000 na hivi sasa ninavyozungumza Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo yuko India kwa ajili ya kufatilia jambo hili hili kuhakikisha kwamba tunapata soko la uhakikia la wakulima wa mbaazi ili kuondokana na changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili pia kupitia TARI na MDT ambayo ni taasisi inayo jishughulisha na masuala ya masoko ya mazao, tumeendelea kutoa elimu na mafunzo juu ya matumizi ya ziada ya mbaazi ikiwemo lishe lakini pamoja na matumizi mengine ya viwanda kwa ajili ya kuongeza soko la zao hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Muhogo tunao mkakati wa kitaifa wa kuendeleza zao la muhogo wa mwaka 2020 mpaka 2030 ambao ndani yake pia umeainisha mikakati mbalimbali ikiwemo kuwahusisha watu wenye viwanda kwa ajili kutengeneza wanga kupitia muhogo, industrial of starch wanaita ili tuongeze soko la muhogo wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tupo katika mawasiliano na ubalozi wa China, Rwanda na Burundi kuongeza wigo mpana wa soko la muhogo ili kuwaondolea changamoto wakulima juu ya upatikanaji wa uhakika wa soko la muhogo.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza nataka kujua hao wanafunzi 1,907 waliorejea shuleni ni asilimia ngapi ya wanafunzi wote ambao walikatisha masomo na walipaswa warejee shuleni?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nataka kujua kuna haja gani ya kuwaacha watoto nyumbani kwa kipindi cha miezi takribani minane tangu wafanye mtihani wa form four mpaka akajiunge na form five, pale pana muda mrefu; kuna sababu gani ya kuacha huo muda kwa sababu kutoka na matokeo ya sensa inaonesha drop out pia zinatokea hapo kwa kiasi kikubwa kwa sababu watoto wanakaa nyumbani muda mrefu, kwa nini muda ule usipunguzwe?

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili kama ulivyosema swali la kwanza linahusu takwimu. Naomba Mheshimiwa Mbunge aridhie baada ya kipindi cha maswali hapa Bungeni au baada ya Bunge tuweze kukutana kuweza kukokotoa hii percentage.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anataka kufahamu mkakati wa Serikali juu ya kupunguza muda wa wanafunzi kusubiri kujiunga na kidato cha tano pamoja na vyuo vingine.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna kipindi cha zaidi ya miezi saba baada ya wanafunzi kufanya mtihani wa kidato cha nne ili waweze kujiunga aidha na kidato cha tano au na vyuo vingine vya kati.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki tunafanya mambo kadhaa ndio maana muda unakuwa mrefu, baada ya mithani kufanyika mwezi wa 11 zoezi la ukusanyaji wa zile script ambazo zimetumika kujibia mitihani huwaga zinakusanywa, lakini baada ya hapo tunakwenda kwenye zoezi la usahihishaji, tukimaliza usahihishaji tunakwenda kwenye zoezi sasa la uteuzi wa wanafunzi, lakini baadae hufanya maandalizi kwa ajili ya wanafunzi hawa sasa kuwapokea kwenye vituo vyetu vya shule mbalimbali. Kwa hiyo, shughuli ambazo zinafanywa katika kipindi hicho ni hizo.

Mheshimiwa Spika, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge Serikali imejidhatiti na kujipanga kwa dhati kuhakikisha kwamba tunapunguza muda huu ambapo sasa tumeanza utaratibu wa kufanya e-Marking kwenda kidato cha nne, tulikuwa tumeanza na darasa la saba kwa mithani ya darasa la saba, lakini sasa tunakwenda na hii mithani ya darasa la nne, tumeanzisha mfumo wa e-Marking ambao utapunguza muda wa usahihishaji, lakini eneo la pili katika upanganji vilevile tumeanzisha mfumo ambao unajulikana kama Management Information System ambao nao vilevile utapunguza muda wa upangaji au uteuzi ule wa wanafunzi kujiunga katika maeneo mbalimbali.

Kwa hiyo, tunapokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge wa kupunguza muda huo ili tuweze kuufanyia kazi sawasawa. Ninakushukuru sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Katika Manisapaa ya Mtwara Mikindani, stand ya mabasi makubwa iliyopo eneo la Chipuputa hali ya miundombinu yake ni mbaya, mvua ikinyesha maji yanajaa wasafiri wanapata shida. Nataka kujua tu kauli ya Serikali, watarekebisha lini ili stand ile iweze kutumika kwa matumizi ambayo yamekusudiwa? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Tunza kwa kufuatilia maendeleo ya wananchi wa Mtwara, lakini nimhakikishie kwamba tumetoa maelekezo kwa Wakurugenzi wote wa Halmashauri zetu kuhakikisha yale maeneo ambayo ni vipaumbele ambayo yanagusa moja kwa moja maslahi ya wananchi zikiwemo stand, kufanya tathmini kuona uwezekano wa kufanya matengenezo kwa kufanya mapato ya ndani au kuandika maandiko maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani kufanya tathmini hiyo au kufanya matengenezo au kuleta maombi kwa ajili ya kufanya kupitia Serikali Kuu. Ahsante.