Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Aeshi Khalfan Hilaly (1 total)

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza; je, Serikali iko tayari kukisaidia Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Pwani (CORECU) ili kiweze kujijenga na kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Pwani hasa wakulima wa korosho wa Wilaya ya Mkuranga waweze kuuza korosho zao kwa bei nzuri lakini pia kupata pembejeo ya sulphur kwa kuwasaidia Chama Kikuu cha Ushirika (CORECU) kulipa deni wanalodaiwa na Benki ya CRDB?
La pili, kuwasaidia Chama Kikuu cha Ushirika (CORECU) kuweza kuyatwaa tena maghala yake yaliyomilikiwa na watu binafsi yaliyopo kule Ukonga, Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inasaidia na imekuwa ikikaa mara kwa mara na CORECU ili kukabiliana na changamoto mbalimbali katika kusaidia wakulima wa korosho katika Mkoa wa Pwani, ikiwa ni pamoja na wanaotoka katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunge. Tayari Wizara imeisaidia CORECU kuweza kulipa sehemu kubwa ya deni ambalo wanadaiwa na CRDB. CRDB walikuwa wanadai CORECU shilingi bilioni 3.5, lakini Serikali ikawasiliana na BOT ili kuweza kulipa asilimia 75 ya principal sum ya deni ambalo walikuwa wanadaiwa kwa sababu BOT alikuwa ni guaranter katika mkataba wa deni lile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tayari imeshalipwa bilioni 1.2 na sasa hivi tunavyoongea bado CORECU wanadaiwa bilioni 2.4, lakini bado tunaendelea kuongea na CRDB ili waweze kuangalia namna ya ku-restructure lile deni ili Chama cha Ushirika cha CORECU waweze kulipa kwa muda mrefu zaidi wasije wakauziwa mali zao. Vilevile, Wizara kwa kushirikiana na Bodi ya Korosho imejiandaa kuhakikisha kwamba pembejeo zinapatikana kwa wakulima wote wa korosho hususan pembejeo ya sulphur kwa ajili ya mikorosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, linahusu maghala ambayo yanamilikiwa. Nimechukua ombi la Mheshimiwa Mbunge na tayari alishafika ofisini kufuatilia hili, nimweleze tu kwamba majadiliano yanaendelea ndani ya Wizara kuangalia ni namna gani bora ya kuweza kurudisha yale maghala kwa wenyewe halali ambao ni Chama cha Ushirika cha CORECU. Ahsante.