Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Abdallah Hamis Ulega (4 total)

MHE. ABDALLAH H. ULEGA aliuliza:-
Je Serikali imejipangaje kuwafidia au kuwapa kifuta machozi wananchi wa Kata za Magawa na Msonga katika vijiji vya Makumbaya, Magewa na Msonga ambao mikorosho kwenye mashamba yapatayo ekari 1000 imeangamia kutokana na ugonjwa wa ajabu na kuwaacha wananchi hawana kitu na hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya maeneo wananchi wanaopatwa na majanga kama haya wamekuwa wakilipwa fidia au hata kifuta machozi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, KILIMO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niamba ya Waziri wa Kilimo Mifugo na Uvuvi, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Hamis Ulega, Mbunge wa Mkuranga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida Serikali haina utaratibu wa kulipa fidia ya athari za maafa, ila ina wajibu wa kuwahudumia wananchi wake wanapokumbwa na majanga. Wizara yangu ilipata taarifa za kuwepo kwa ugonjwa huo na kuelekeza wataalam kufanya utafiti ili kubaini sababu, namna ya kuzui pamoja na tiba. Baada ya utafiti huo, iligundulika kuwa na ugonjwa huo unasababishwa na kuvu (fungus) aina ya Fussarium wilt. Hivi sasa Taasisi yetu ya Utafiti ya Naliendele inaendelea na majaribio ya viuatilifu vitakavyoweza kutibu ugonjwa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango uliopo wa kuwasaidia wakulima kama ilivyo utaratibu wa Serikali ni kusambaza miche mipya ya korosho inayohimili ugonjwa katika maeneo yanayoathirika baada ya kupata mahitaji halisi kutoka Halmashauri. Aidha, namshauri Mheshimiwa Mbunge na Halmashauri ya Mkuranga kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kufanya tathmini ya kina ili kuona kama athari za ugonjwa huo zina tishio la watu kufa njaa, ili utaratibu wa kuomba chakula cha msaada ufanyike mara moja kuokoa maisha ya watu wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada hizo kupitia Bodi ya Korosho Tanzania, taarifa za tahadhari zimeanza kutolewa kupitia vyombo vya habari kwa wakulima ambapo pamoja na mambo mengine, wakulima wameaswa kuteketeza mikorosho iliyoathirika na ugonjwa huo na kuepuka kuhamasisha udongo kutoka kwenye naeneo yaliyoathirika kwenda kwenye maeneo mengine.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA aliuliza:-
Je ni lini Serikali itawasaidia wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kwa kuwaunganisha kwa barabara ya moja kwa moja kutoka Mkuranga - Kisarawe - Kibaha bila ya kupitia Mkoa wa Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasialiano napenda kujibu swali la Mheshimwia Abdallaha Hamis Ulega, Mbunge wa Mkuranga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya za Mkuranga, Kisarawe na Kibaha zimeunganishwa na barabara za lami kupitia Dar es Salaam kutokana na sababu za kijiografia. Aidha, Wilaya za Kibaha na Kisarawe zinaunganishwa na barabara ya Kiluvya - Mpuyani yenye urefu wa kilometa 22, na Wilaya za Kisarawe na Mkuranga zinaunganishwa na barabara ya lami kupitia Mbagala - Charambe yenye urefu wa kilometa 29.
Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya Wilaya za Mkuranga na Kibaha yapo kwenye barabara kuu za Dar es Salaam – Kibiti – Lindi; na Dar es Salaam - Chalinze - Mbeya hadi Tunduma na barabara hizi zinapitika na zipo kwenye hali nzuri. Aidha, barabara ya moja kwa moja ya Mkuranga - Kisarawe -Kibaha, itawekwa katika mipango ya baadae ya Serikali kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA aliuliza:- Je, ni hatua gani madhubuti Serikali itachukua kwa kampuni zinazoshinda tender (zabuni) za ununuzi wa korosho lakini haziwalipi wakulima kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Hamis Ulega, Mbunge wa Mkuranga kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya masuala ya msingi katika miongozo ambayo hutolewa na Serikali kupitia Bodi ya Korosho Tanzania ni kuwataka wanunuzi wa korosho kulipia kwa wakati korosho wanazoshinda kwenye mnada. Hata hivyo, baadhi ya wanunuzi hukiuka masharti hayo kwa visingizio mbalimbali ikiwemo kushuka kwa ubora wa korosho tofauti na ule uliopo kwenye sales catalogue na kushuka kwa bei ya korosho katika masoko ya nje. Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Bodi ya Korosho imekuwa ikihimiza wanunuzi kufuata sheria, kanuni za taratibu zilizowekwa na mamlaka husika. Aidha, Serikali kupitia Sheria ya Korosho Namba 18 ya mwaka 2009 kifungu cha 17 na kanuni za mwaka 2010 kanuni ya 33, itafungia kampuni yoyote ambayo inafanya biashara ya korosho nchini endapo itakiuka sheria na kanuni ikiwemo ya kutowalipa wakulima kwa wakati ili kubaki na makampuni yanayotii sheria. Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Bodi ya Korosho imefanya maboresho na kutoa mwongozo ulioanza kutumika msimu wa mwaka 2016/2017 kwa kila mnunuzi kuweka dhamana ya fedha taslimu au hundi ya benki kulingana na kiasi cha korosho alizonunua kama dhamana itakayotumika kuwalipa wakulima endapo mnunuzi akishindwa kuwalipa wakulima. Kiwango cha chini ni kununua tani 50, mnunuzi akinunua kati ya tani 50 na 100 atalazimika kulipa shilingi milioni 50 kama dhamana. Kati ya tani 101 na tani 1000 dhamana yake ni shilingi milioni 100 na zaidi ya tani 1001 dhamana yake ni shilingi milioni 300. Dhamana hiyo huchukuliwa mara baada ya Bodi ya Korosho na wahusika wote vikiwemo Vyama vya Ushirika kujiridhisha kuwa mnunuzi alikiuka taratibu na pia adhabu nyingine zinaweza kuchukuliwa dhidi ya kampuni husika.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA aliuliza:-
Je, Serikali ipo tayari kuwalipa fidia wananchi waliowekewa alama za ‘X’ kwenye nyumba zao katika Barabara ya Mkuranga kwenda Kisiju?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Hamis Ulega, Mbunge wa Mkuranga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na Sheria ya Barabara Namba 13 ya mwaka 2007 iliyopitishwa na Bunge lako Tukufu, eneo la hifadhi ya barabara kwa barabara kuu na barabara za mikoa limeongezeka kutoka mita 22.5 zilizotajwa katika Sheria ya Barabara ya mwaka 1967 hadi mita 30 kila upande kutoka katikati ya barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Mkuranga hadi Kisiju yenye urefu wa kilometa 46 ni miongoni mwa barabara za mikoa zilizopo chini ya usimamizi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Katika kutimiza matakwa ya Sheria ya Barabaa ya mwaka 2007 Wakala wa Barabara Tanzania ulifanya zoezi la utambuzi wa mali zilizopo ndani ya hifadhi ya barabara kuu na barabara za mikoa nchini nzima ikiwemo Barabara ya Mkuranga hadi Kisiju. Lengo la kuweka alama ya ‘X’ ni kuwajulisha na kuwatahadharisha wananchi juu ya ongezeko la eneo la hifadhi ya barabara ili wasifanye maendeleo mapya kwenye maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya nyumba zilizowekwa alama ‘X’ kuna ambazo zimo katika hifadhi ya barabara ya mita 22.5 kila upande wa barabara ambapo wamiliki wake walipewa notice ya kuziondoa bila kulipwa fidia kwa kuwa walivamia eneo la hifadhi ya barabara. Kwa zile ambazo zimo kati ya mita 22.5 hadi 30 kila upande wamiliki wake wanastahili kulipwa fidia. Kwa sasa wananchi hawa hawatakiwi kufanya maendelezo yoyote katika maeneo hayo ingawa hawalazimiki kuomba wala kuondoa mali zao mpaka hapo Serikali itakapolihitaji eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Aidha, kabla Serikali haijatwaa eneo hilo uthamini utafanyika na wananchi wanaostahili kulipwa fidia watalipwa.