Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Abdallah Hamis Ulega (117 total)

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kukarabati malambo ya Vijiji vya Makomariro 2, Kyandege, Mugeta, Mariwanda, Kihumbu, Kisangwa, Sanzete, Salama A, Salama Kati na Nyangaranga ambayo yamejaa magugu maji na mengine kina chake kimepungua?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilichimba malambo katika Vijiji vya Makomariro 2, Kyandege, Mugeta, Mariwanda, Kihumbu, Kisangwa, Sanzete, Salama A, Salama Kati na Nyangaranga kwa ajili ya kutatua matatizo ya ukosefu wa maji ya kunyweshea mifugo na kwa matumizi ya binadamu. Ni kweli malambo hayo kwa sasa yamejaa magugu maji na tope.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali imekuwa ikiwahamasisha wananchi wa vijiji husika kuyaweka malambo hayo katika mipango yao ya bajeti na kuiwasilisha Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ili yawekwe na kutengewa fedha kwenye mpango wa bajeti ya mwaka husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa malambo hayo, Halmashauri ya Bunda ilifanya tathmini ili kujua gharama halisi ya ukarabati unaohitajika kwa ajili ya kuweka kwenye bajeti ya mwaka 2018/2019. Ukarabati huo utagharimu jumla ya Sh.36,825,600 kwa mchanganuo ufuatao: Lambo la Kyandege litahitaji Sh.25,618,350, Mugeta Sh.97,870,400, Sanzete Sh.36,286,000, Salama A Sh.25,926,000, Salama Kati Sh.46,315,850, Makomariro Sh.25,926,000, na Kihumbu Sh.108,883,000. Ukarabati wa malambo haya umepangwa kufanywa katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili malambo yaliyochimbwa au kukarabatiwa yaweze kuwa endelevu, Serikali inatoa ushauri kwa vijiji husika kuunda Kamati za Uendelezaji wa Malambo ambazo zitahusika na utungaji wa Sheria ndogondogo za utunzaji wa malambo hayo.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Suala la ufugaji samaki lina faida nyingi kwa wananchi kama kujiongezea kipato na kupata kitoweo lakini wananchi wa Kata za Ninde, Kala, Wampembe na Kizumbi walioko kando ya Ziwa Tanganyika hawafugi samaki kwa kukosa elimu:-
Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam kutoa elimu ya ufugaji samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa shughuli za ufugaji wa samaki zina faida nyingi kwa wananchi zikiwemo kujipatia ajira, lishe na kipato. Wilaya ya Nkasi ni moja ya Wilaya zenye mazingira na maeneo mazuri kwa ajili ya ufugaji wa samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ina wataalam wa uvuvi saba, wawili kati ya hao wana shahada ya ukuzaji wa viumbe kwenye maji na watano wana diploma zinazohusiana na masuala ya uvuvi na ufugaji wa samaki. Aidha, Kituo cha Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi (doria) cha Kipili kilichopo katika Wilaya ya Nkasi chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kina wataalam watano. Pamoja na shughuli za usimamizi wa rasilimali za uvuvi katika Ziwa Tanganyika, watumishi hao wana jukumu la kusimamia shughuli za ufugaji wa samaki ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za ugani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza kasi ya utoaji elimu ya ufugaji wa samaki katika ukanda wa mwambao mwa Ziwa Tanganyika, Serikali kupitia Wakala wa Elimu ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) ilianzisha kituo cha FETA Kibirizi – Kigoma ambapo mwaka 2015/2016 kilidahili wanafunzi 59 na wanafunzi 29 walihitimu masomo yao na katika mwaka 2016/2017 walidahili wanafunzi 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Kituo cha Ukuzaji Viumbe kwenye Maji kilichopo Manispaa ya Kigoma kwa kushirikiana na Halmashauri zilizoko kwenye ukanda huo kimehamasisha ufugaji wa samaki na kuzalisha vifaranga vya samaki 31,404, ambapo katika mwaka 2016/2017, Wilaya ya Nkasi jumla ya wananchi 70 walipata elimu ya ufugaji wa samaki katika Vijiji vitatu vya Ninde, Msamba, Namansi ambao wameanzisha kikundi kimoja katika Kitongoji cha Chele. Katika Kata ya Kala jumla ya watu 270 kutoka Vijiji sita vya Kala, Tundu, Kilambo, King’ombe na Mlambo wamepata elimu ya ufugaji wa samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na viongozi wenzake katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi katika kuweka vipaumbele na uhamasishaji wa ufugaji wa samaki ili wataalam waliopo waendelee kuhamasisha ufugaji wa samaki katika maeneo yaliyoainishwa na watumishi kutoka Wizarani tutahakikisha kwamba tunakwenda Nkasi kushirikiana nao katika kutoa huduma za ugani katika masuala ya ufugaji wa samaki. Aidha, vijana washauriwe kujiunga na mafunzo ya ufugaji wa samaki katika Kituo cha Wakala wa Elimu Mafunzo ya Ufundi (FETA) kilichopo Kibirizi – Kigoma na hatimaye waweze kujiajiri katika shughuli za ufugaji wa samaki kwa lengo la kujipatia ajira, lishe na kipato.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-
Serikali imeondoa tozo mbalimbali zilizokuwa kero kwa wananchi katika sekta ya uvuvi lakini bado kuna mkanganyiko ni tozo zipi zimefutwa na zipi zinaendelea.
(a) Je, Serikali inaweza kuainisha aina ya tozo zilizoondolewa katika sekta ya uvuvi?
(b) Je, ni lini Serikali itatoa mwongozo kwa watendaji wa Halmashauri juu ya mabadiliko hayo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na kutekeleza Sera ya Uvuvi ya mwaka 2015 ambayo pamoja na mambo mengine inaelekeza kuweka mazingira mzuri katika kuwezesha wavuvi na wawekezaji kuendesha biashara ya uvuvi kwa ufanisi.
Aidha, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati akifungua rasmi Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 20 Novemba, 2015 katika hotuba yake alielekeza kupitia na kuangalia tozo zote ambazo ni kero kwa wananchi ili ziondolewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 inaelekeza kuwezesha wavuvi wadogo kwa kuwaondolea kero mbalimbali zikiwemo tozo zisizo na tija. Ili kutekeleza maelekezo haya, wizara yangu katika Bunge la Bajeti ya mwaka 2017/2018 ilitangaza kuondoa ada na tozo mbalimbali ambazo zilionekana kuwa kero katika sekta ya uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ada na tozo zilizoondolewa katika sekta ya uvuvi ni kama ifuatavyo:-
• ushuru wa kaa hai (waliozalishwa na kunenepeshwa) wanaouzwa kwenda nje ya nchi.
• Tozo ya cheti cha afya baada ya kukagua mazao ya uvuvi shilingi 30,000.
• Ada ya ukaguzi wa kina wa kiwanda/ghala kila robo mwaka shilingi 100,000.
• Tozo ya usafirishaji samaki yaani movement permit kuanzia kilo 101 hadi kilo 1000 shilingi 5,000; kilo 1001 hadi kilo 5000 ni shilingi 10,000; kilo 5001 hadi kilo 9999 shilingi 30,000; zaidi 10,000 na zaidi shilingi 50,000.
• Ada ya usajili wa chombo cha uvuvi chini ya mita 11 kwa wavuvi wadogo shilingi 20,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha mabadiliko ya tozo katika sekta ya uvuvi inatekelezwa na watendaji wa Halmashauri, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Wizara ya TAMISEMI imeshatoa maelekezo kwa Halmashauri husika kusitisha mara moja tozo ambazo zimefutwa na Serikali. Aidha, Wizara Wizara inafanya marekebisho katika Kanuni za Uvuvi za mwaka 2009 ili kuendana na mabadiliko hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kupitia Halmashauri zetu kuhakikisha kuwa maagizo haya kuhusu tozo zilizoondolewa na Serikali yanatekelezwa.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Serikali kupitia Ilani ya CCM ya 2015 – 2020, ahadi namba 25(d) iliwaahidi vijana wafugaji kuwa itatoa dhamana ya mikopo kwenye asasi za fedha.
(a) Je, Serikali imeandaa mkakati gani wa kuwawezesha vijana wafugaji kuunda vyama vya ushirika ili waweze kunufaika na ahadi hiyo ya CCM?
(b) Je, Serikali inayo orodha ya vikundi vya vijana wafugaji ambao wamejiunga na vyama vya ushirika ambao wameweza kunufaika na utaratibu wowote ulioandaliwa na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maria Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati ulioandaliwa na Serikali katika kuwawezesha vijana wafugaji kuunda vyama vya ushirika ni pamoja na kushirikisha Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvivi, Ofisi ya Rais TAMISEMI na wadau wengine katika kuhamasisha wafugaji, hususan vijana kuanzisha, kufufua na kujiunga na vyama vya ushirika vilivyopo. Uhamasishaji huo umefanyika kupitia mikutano na kampeni katika mikoa mbalimbali ikiwemo mikoa ya Tanga, Shinyanga, Mwanza, Iringa, Rukwa, Njombe, Manyara, Dodoma, Lindi na Mtwara ambapo wananchi walihamasika na kujiunga katika ushirika. Vilevile Wizara imeviunganisha vyama vya ushirika na wadau mbalimbali katika kuhamasisha ufugaji na uboreshaji wa mifugo. Baadhi ya wadau hao ni Oxfam, Care International na CARITAS.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ifuatayo ni idadi ya wafugaji waliohamashishwa kujiunga na vyama vya ushirika katika mikoa mbalimbali; Tanga jamii ya Wamasai na Wabarbaig wapatao 253; Njombe na Lindi wafugaji 265 walipatiwa elimu ya ushirika; Singida vikundi 62 vyenye wanachama 1,397 vilipatiwa elimu; Rukwa jumla ya wananchi 968 walihamasika kwa kujiunga kuanzisha vikundi vya ushirika; Dodoma kuna vikundi vipatavyo 338 ambavyo vinaundwa na rika mbalimbali; Shinyanga kuna vikundi 47, kati ya hivyo viwili vinajishughulisha na unenepeshaji wa ng’ombe na usindikaji wa ngozi. Taasisi za BRAC, Good Neighbourhood na World Vision zinatoa ufadhili wa mafunzo, ujenzi wa mabanda ya mfano, mifugo ya kuanzia kama mbegu pamoja na mashine za kuchakata ngozi kwa vikundi vya Mkoa wa Dodoma.
MHE. ALEX R. GASHAZA Jimbo la Ngara lina mifugo mingi hususan ng’ombe na mbuzi, lakini kuna tatizo kubwa la maeneo ya kunyweshea mifugo kwa maana ya malambo/ mabwawa kwa ajili ya kunyweshea mifugo.
Je, ni lini Serikali itaanza uchimbaji na ujenzi wa malambo/mabwawa kwa ajili ya kunyweshea mifugo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, kwanza napenda kumpa pole sana rafiki yangu, Mheshimiwa Alex Raphael Gashaza, mpiganaji, Mbunge wa Ngara kwa maafa yaliyowapa Wanangara, lakini pia naomba kujibu swali sasa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Wilaya ya Ngara ina mifugo mingi ambapo pia hali hii inasababishwa na mifugo kuhamia kutoka nchi jirani bila kufuata utaratibu. Takwimu za mwaka 2016 zinaonesha Wilaya ya Ngara ina ng’ombe wa asili 70,000, ng’ombe wa maziwa 2,872 na mbuzi wa asili 190,000, mbuzi wa maziwa 169,000 na kondoo wa asili 14,600.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo jitihada mbalimbali ambazo zimechukuliwa na Serikali ili kukabiliana na upungufu wa maji kwa mifugo. Serikali imekuwa ikitekeleza mkakati wa kujenga malambo ya maji kwa ajili ya mifugo katika maeneo mengi nchini tangu mwaka 2001/2002 kwa kupitia bajeti ya Wizara na kupitia miradi shirikishi ya kuendeleza kilimo katika Wilaya ya Ngara pia katika miradi iliyoibuliwa na jamii yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika juhudi hizo, Halmashauri ya Wilaya ya Ngara kupitia ufadhili wa TASAF Awamu ya Tatu, inatarajiwa kujenga mabirika manne ya kunyweshea mifugo katika vijiji vya Magamba, Mumuhamba, Munjebwe na Nterungwe. Aidha, mradi unajenga bwawa moja katika kijiji cha Kasulo na miradi yote ya maji ya mifugo hadi kukamilika itagharimu jumla ya shilingi 135,569,900. Ujenzi wa malambo yote umekamilika, kilichobakia ni ujenzi wa mabirika ya kunyweshea mifugo. Jumla ya watu takribani 685 watafaidika na miradi hii.
ZAINAB A. KATIMBA (K.n.y. MHE. MOSHI S. KAKOSO) aliuliza:-
Wavuvi wadogo wadogo wa Ziwa Tanganyika wana tatizo la vitendea kazi.
Je, ni lini Serikali itawapatia wavuvi hao vitendea kazi vya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako, kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, kumshukuru Mheshimiwa Spika, wananchi wenzangu wa Mkuranga na kwa namna ya kipekee kabisa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuniamini kushika nafasi hii ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, naomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, nijibu swali la Mheshimiwa Moshi Kakoso, Mbunge wa Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuhamasisha wadau wa uvuvi, ikiwemo sekta binafsi na jamii ya wavuvi wenyewe kuwekeza katika matumizi ya zana bora za uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha mapato yao, baadhi ya mikakati iliyotekelezwa ni kuwawezesha wavuvi wadogo kuanzisha vyama vya ushirika vya msingi kupitia halmashauri husika na pia wawekezaji wakubwa kuwekeza kwenye viwanda vya kutengeneza boti na zana mbalimbali za uvuvi hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ziwa Tanganyika, tunacho Kituo chetu cha Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) pale Kibirizi Kigoma, ambapo tunayo mipango kama Serikali kukiimarisha ili kiweze kuunda boti za kisasa na pia kuendelea kutoa mafunzo na elimu inayohusu sekta ya uvuvi kwa wanafunzi na jamii za wavuvi na wadau wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inatekeleza Sheria ya VAT ya mwaka 2007 ambayo imetoa msamaha wa kodi ya zana za uvuvi na malighafi nyingine ikiwemo injini za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu na vifungashio vyake. Vilevile katika jitihada nyingine za kuwasaidia wavuvi, Serikali hii ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, katika mwaka 2015/2016 ilitenga jumla ya fedha shilingi milioni mia nne ambapo jumla ya injini za boti 73 zilinunuliwa na katika hizo boti 49 zilishachukuliwa na vikundi vya wavuvi mbalimbali nchini kupitia Halmshauri zao katika mtindo wa ruzuku ambapo Serikali inachangia asilimia 40 na vikundi vya wavuvi vinachangia asilimia 60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi sasa tunazo boti takribani 24 ambazo zinawasubiri wavuvi mbalimbali waliopo nchini ikiwa ni pamoja na wavuvi walioko Mpanda na Ziwa Tanganyika lote kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shime kwa Waheshimiwa Wabunge, tuhamasishe vikundi hivi vya wavuvi, mashine hizo bado tunazo, waweze kuja kupitia halmashauri zao kwa kufuata utaratibu kuzipata na kuweza kuimarisha shughuli zao za uvuvi kwa ajili ya kujipatia kipato zaidi.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI aliuliza:-
Shamba la malisho lililopo katika Kata ya Shishiyu Wilayani Maswa linamilikiwa na Serikali lakini halitumiki ipasavyo:-
Je, Serikali Kuu haioni haja ya kulirejesha shamba hilo kwa Halmashauri ya Wilaya ili lipangiwe matumizi mengine?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha kupumzishia mifugo (holding ground) cha Shishiyu kina ukubwa wa hekta 4,144 na ni kati ya vituo 28 vilivyotengwa nchi nzima kwa mujibu wa Sheria ya Magonjwa ya Wanyama Na. 17 ya mwaka 2003 kwa ajili ya kukusanya na kupumzisha mifugo inayotoka minada mbalimbali kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa kabla ya kusafirisha mifugo hiyo kwenda katika viwanda vya kuchinja na kuchakata nyama au kusafirisha kwenda nje ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, uwepo wa vituo vya kupumzishia mifugo ni hitaji la Kimataifa katika biashara ya mifugo. Zipo sheria mbalimbali za Kimataifa zinazolazimisha uwepo wa maeneo haya, yanayolenga utoaji huduma unaozingatia viwango ambazo zinasimamiwa na Shirika la Afya ya Wanyama ulimwenguni - OIE na makubaliano ya Kimataifa ya afya ya wanyama na mimea (Sanitary and Phytosanitary (SPS) chini ya Shirika la biashara la Kimataifa (WTO).
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili pia hutumika kama kituo cha karantini kwa ajili ya kuchunguza magonjwa, hususan yale ya milipuko yanapojitokeza hasa kutokana na Kanda ya Ziwa kuwa na mifugo mingi na baadhi ya mikoa katika Kanda hii inapakana na nchi jirani hivyo ni rahisi ka magonjwa ya wanyama ya milipuko kujitokeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kuna mwingiliano mkubwa wa wanyama wafugwao na wanyama pori kutoka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Pori Tengefu la Maswa kutokana na umuhimu wa kituo hiki kwa ajili ya biashara ya mifugo ndani na nje ya nchi. Hivyo, siyo vema kubadilisha matumizi na madhumuni ya kuanzishwa kwa kituo hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, eneo hili litaendelea kubaki chini ya usimamizi wa Serikali Kuu kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili eneo hili liweze kutumiwa na wadau wote waliopo kwenye mnyororo wa kuongeza thamani (value chain) ya mifugo na mazao yake.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-
(a) Ranchi ya NARCO Mbarali ilianzishwa kwa ajili ya mifugo; Je, ni kwa nini eneo hilo sasa linatumika kwa kilimo?
(b) Migogoro ya wakulima na wafugaji Mbarali imekuwa ni mingi; je, kwa nini Serikali isitoe eneo la Ranchi ya NARCO Mbarali ili litumike kwa ajili ya malisho ya mifugo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Ranchi ya NARCO iliyopo Mbarali inajulikana kwa jina la Ranchi ya Usangu na ina ukubwa wa hekta 43,727 ambazo zimegawanywa katika vitalu 16 vyenye ukubwa wa hekta kati ya 2,000 na 3,000. Kutokana na maelekezo ya Wakala wa Baraza la Mawaziri Namba (2) wa mwaka 2002, vitalu vya Ranchi ya Usangu vimekodishwa kwa mkataba maalum kwa wawekezaji wa Kitanzania kwa ajili ya kuendeleza ufugaji wa kisasa na kibiashara ili kuwa na ufugaji wenye tija. Kwa sasa vitalu vya wawekezaji hao vina jumla ya ng’ombe 2,722, mbuzi 1,145 na kondoo 500.
Mheshimiwa Spika, shughuli za uendelezaji mifugo zinaendana na kilimo cha malisho ya mifugo na mazao mengine ambayo mabaki yake hutumika kwa kulishia mifugo. Shughuli za uendeshaji wa nyanda za malisho ni kipengele muhimu kulingana na mkataba wa uwekezaji. Aidha, unenepeshaji wa mifugo hufanyika ndani ya vitalu vya wawekezaji ili kuvuna mifugo kwa muda mfupi na hivyo mabaki ya mazao hutumika kulisha mifugo kama sileji na hei.
Serikali kupitia NARCO inafanya tathmini ya vitalu hivyo na wale watakaobainika kukiuka makubaliano, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwa ni pamoja na kuvunja mikataba ya ukodishaji ili kuwapatia wawekezaji wengine wenye uwezo wa kuwekeza kulingana na mikataba.
(b) Mheshimiwa Spika, kutokana na mkataba wa uwekezaji, Ranchi hiyo haiwezi kugawiwa kwa wananchi, kwa kuwa kuruhusu maeneo ya Ranchi kutumiwa na mifugo kwa ajili ya malisho itakuwa ni ukiukwaji wa sheria ya mkataba kati ya wawekezaji na NARCO. Aidha, kuruhusu uingizaji wa mifugo ndani ya Ranchi kutasababisha maambukizi ya magonjwa kwa mifugo ya wawekezaji.
MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Sekta ya uvuvi bado haijatumika kikamilifu kulipatia Taifa pato na kuwaondoa Watanzania hususani wavuvi katika dimbwi la umaskini.
(a) Je, ni lini Serikali itaweka jitihada za kusaidia wavuvi hasa wale wanaojihusisha na uvuvi wa Bahari Kuu?
(b) Je, ni lini Serikali itatoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wavuvi wadogo wadogo ili waweze kuvua katika Bahari Kuu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Mchinga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutoa kipaumbele kwa sekta ya Uvuvi nchini kwa kutekeleza mikakati yenye lengo la kuendeleza wavuvi nchini ili waweze kupata ajira, lishe, kipato na kuchangia katika Pato la Taifa. Kwa mwaka 2016 sekta ya Uvuvi imechangia asilimia 2.0 katika Pato la Taifa na imekua kwa asilimia 4.2.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jitihada za kuwasaidia wavuvi wadogo hususani wale wanaojihusisha na uvuvi wa Bahari Kuu Serikali imeanza kuweka vifaa maalum vya kuvutia samaki (Fish Aggregating Devices - FADs) ili kuwasaidia wavuvi kupata samaki wengi na kutumia muda mfupi katika uvuvi. Hadi sasa jumla ya FADs 77 za mfano zimewekwa katika maeneo mbalimbali. Vilevile Serikali imetoa mafunzo kwa wavuvi wadogo ili waweze kuvua katika Bahari Kuu ambapo hadi sasa jumla ya wavuvi 150 wakiwemo 83 wa Ukanda wa Pwani ya Bahari wa Hindi.
• Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo inatoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wakulima wakiwemo wavuvi na wafugaji ili waweze kununua zana bora za uvuvi. Aidha, Serikali imeanzisha Dirisha la Kilimo katika Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB). Mikopo hiyo inatolewa kupitia vyama vya ushirika ambayo pamoja na majukumu mengine inatoa pia mikopo ya masharti nafuu kwa watu wanaojishughulisha na sekta za kilimo, mifugo na uvuvi. Ili kuweza kukidhi masharti ya kupata mikopo hiyo, Serikali inaendelea kuwahamasisha wavuvi kujiunga katika Vyama vya Ushirika vya Msingi wa Wavuvi ili kuwa na nguvu ya pamoja na kuweza kukopesheka.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA (K.n.y MHE. HASNA S. K. MWILIMA) aliuliza:-
Shughuli kubwa za kiuchumi kwa wananchi wa Ukanda wa Ziwa Tanganyika ni uvuvi lakini nyavu zimekuwa zikikamatwa na kuchomwa moto.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia wavuvi hao nyenzo au vifaa vya kisasa vya uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutekeleza mikakati yenye lengo la kuboresha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya uvuvi ili kuwawezesha wavuvi wakiwemo wa Ukanda wa Ziwa Tanganyika kufanya uvuvi endelevu na wenye tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeondoa kodi kwenye zana na malighafi za uvuvi zikiwemo engine za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu na vifungashio kupitia Sheria ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya mwaka 2007. Aidha, kupitia Umoja wa Ushuru wa Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (The East African Community Common External Tariff) engine za uvuvi na malighafi zinazotumika kutengeneza zana mbalimbali za uvuvi na viambata vyake kwa maana ya fishing gear accessories 10% na outboard engine 0%) zimepewa punguzo la kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo inatoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wananchi wakiwemo wavuvi ili waweze kununua zana bora za uvuvi. Hivyo wavuvi wahamasishwe kujiunga katika Vyama vya Ushirika ili kuwawezesha kupata mikopo hiyo.
Vilevile Serikali inatekeleza mpango wa kutoa ruzuku ya zana za uvuvi, ambapo wavuvi wenyewe huchangia 60% na 40% iliyobaki ya gharama huchangiawa na Serikali. Hadi sasa engine 73 zimenunuliwa kupitia mpango huu, nakati ya hizo engine 49 zimelipiwa na kuchukuliwa na vikundi vya wavuvi vilivyokidhi vigezo vikiwemo vitatu kutoka katika Wilaya ya Kalambo na kimoja kutoka katika Wilaya ya Sumbawanga.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-
Sekta ya Uvuvi ni moja ya maeneo ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inayaona kuwa yanaweza kukuza uchumi kwa kuongeza Pato la Taifa, kupunguza umaskini na tatizo la ajira.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wavuvi wadogo wadogo Wilayani Kilwa kwa kuwapatia zana za kisasa za uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutekeleza mikakati yenye lengo la kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuwawezesha wavuvi wadogowadogo wakiwemo wa Wilaya ya Kilwa kupata zana za uvuvi kwa bei nafuu ili kufanya uvuvi endelevu na wenye tija. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuondoa kodi kwa zana na malighafi za uvuvi zikiwemo engine za kupachika, nyuzi za kushonea, nyavu na vifungashio kupitia Sheria ya VAT ya mwaka 2007.
Vilevile kupitia Chapisho la Pamoja la kodi la Afrika Mashariki engine za uvuvi na malighafi zinazotumika kutengeneza zana mbalimbali za uvuvi na viambata vyake zimepewa punguzo la kodi ili kuwawezesha wavuvi kumudu bei za vifaa hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Programu ya Kutoa Ruzuku kwa Wavuvi, Serikali katika Awamu ya Kwanza ilinunua engine 73 na hadi sasa engine 49 zimelipiwa na kuchukuliwa na vikundi vya wavuvi vilivyokidhi vigezo vikiwemo vikundi 27 kutoka Ukanda wa Pwani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutumia nafasi hii kuomba Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kuhamasisha wavuvi kujiunga kwenye Vyama vya Ushirika vya Msingi ili waweze kunufaika na fursa hii kama wavuvi wengine katika ukanda huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imeanzisha Benki ya Kilimo ambayo pamoja na masuala mengine inaweza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa wavuvi ili kuboresha shughuli zao za kimaendeleo. Kutokana na kuwepo kwa benki hii na taasisi nyingine za kifedha, Serikali inaendelea kuhamasisha wavuvi kote nchini kujiunga katika Vyama vya Ushirika wa Wavuvi ili waweze kukopesheka na kuweza kununua zana za kisasa za uvuvi.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI aliuliza:-
Kwenye bahari na maziwa yetu kuna samaki wa aina mbalimbali kama vile dagaa, furu, uduvi au dagaa mchele na wengine ambao ni wadogo sana.
(a) Je, ni nyavu zenye ukubwa wa size gani zinahitajika kwa ajili ya uvuvi wa aina hizo ndogo ndogo za samaki?
(b) Je, Serikali inafanya utaratibu gani wa kuwapatia wavuvi wa nyavu ndogo ndogo za samaki nyavu zinazohitajika kwa uvuvi huo?
(c) Je, elimu ya kutosha kwa nyavu husika imefanyika kwa kiwango gani hasa kwa wavuvi wanozunguka Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi lenye sehemu (a), (b) na
(c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kila samaki hunaswa kwa kutumia wavu wa aina yake bila kuathiri samaki wengine. Kwa mfano kulingana na kanuni za uvuvi nyavu za kuvulia dagaa baharini zinapaswa kuwa na macho au matundu yenye ukubwa wa milimita 10 na kwa upande wa dagaa wanaovuliwa ziwani ukubwa wa macho au matundu ya milimita nane. Aidha, dagaa huvuliwa nyakati za usiku kwa kutumia mwanga wa taa za karabai.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kuwawezesha wavuvi kupata dhana za uvuvi kwa gharama nafuu ikiwa ni pamoja na kuwaondelea kodi katika dhana na malighafi za uvuvi zikiwemo nyuzi za kushonea nyavu vifungashio na injini za kupachika. Aidha, Serikali inaendelea kuwahimiza wavuvi kujiunga katika vikundi na kuanzisha vyama vya ushirika vya msingi, vyama vya akiba na mikopo (SACCOS) na VICOBA ili waweze kukopesheka na kuweza kununua dhana na vyombo bora vya uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupitia programu ya utoajiwa ruzuku kwa wavuvi Serikali katika awamu ya kwanza ilinunua engine 73 ambapo hadi sasa engine 49 zimelipiwa na kuchukuliwa vikiwemo vikundi 13 kutoka ukanda wa Ziwa Victoria. Vile vile Serikali imeweka mazingira ya kupata mikopo kwa ajili ya kununua dhana bora za uvuvi kwa kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB).
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuwatumia Maafisa wa Idara ya Uvuvi na BMUs imekuwa ikitoa elimu ya kutosha kuhusiana na matumizi endelevu ya nyavu za uvuvi kwa wavuvi wanaozunguka Ziwa Victoria na katika maeneo mengine nchini. Aidha, viongozi wa mikoa na Wilaya wamekuwa wakiongelea suala hili katika hotuba zao wanapofanya ziara za kuwatembelea wavuvi katika maeneo yao.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-
Tanzania ni nchi ya pili kwa kuwa na mifugo mingi Barani Afrika. Je, Serikali haioni ni wakati muafaka wa kupiga marufuku uingizwaji wa nyama kutoka nchi za nje ili kuruhusu ukuaji wa viwanda vya nyama nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Tanzania ni nchi ya pili kwa kuwa na mifugo mingi Barani Afrika baada ya Ethiopia. Aidha kumekuwepo na uingizaji wa nyama ya ng’ombe, nguruwe na kondoo kwa wastani wa tani 2,000 kwa mwaka kuanzia mwaka 2013 hadi 2015. Hata hivyo kiasi hicho kimepungua kuanzia mwaka 2016 tani 1,182.79 na mwaka 2017/2018 tani 1,225 kutokana na kuwepo kwa machinjio na viwanda 23 vyenye uwezo wa kuzalisha tani 44,820.6 za nyama na bidhaa zake kwa mwaka zenye ubora linganifu na nyama inayotoka nje ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2016/2017 jumla ya nyama tani 2,608.93 yenye thamani ya dola za kimarekani bilioni 5,679,217.28 iliuzwa katika nchi za Oman, China, Hong Kong, Dubai na Vietnam. Vilevile idadi ya machinjio nchini kwa sasa ni 1,632 na yana uwezo wa kuchinja nyama kiasi cha tani 625,992 kwa mwaka.
Pia masoko ya nyama inayozalishwa ndani ya nchi yameongezeka ambapo inauzwa katika hoteli za kitalii, maduka maalum (super markets) na migodi yote nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inafanya tathmini ya kina kuhusu biashara ya mifugo na mazao yake ili kujua kwa uhakika kiasi cha nyama kinachoingizwa nchini, masoko na uwezo wa viwanda vya ndani katika kuzalisha nyama na mazao yenye ubora na viwango vya kimataifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali imeendelea kuweka mazingira mazuri na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vya kuzalisha, kuchakata na kusindika nyama na bidhaa zake zenye viwango na ubora unaokubalika. Pia, imeweka mapendekezo ya kuongeza tozo ya uingizaji wa nyama na bidhaa zake ili kuleta ushindani wa haki katika soko la ndani utakaowezesha kukua kwa viwanda vya ndani, kupunguza na hatimaye kuondoa kabisa uingizaji wa nyama kutoka nje ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kulihakikishia Bunge lako tukufu kwamba wizara inaupokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge kwa ajili ya kuufanyia kazi na kwa kuzingatia matokeo ya tathmini tunayoendelea hivi sasa.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunikumbusha, naomba isomeke dola za kimarekani 5,679,217.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-
Mnada wa Magena uliopo Halmashauri ya Mji wa Tarime una miundombinu yote licha ya kufungwa na Serikali bila sababu maalum na kusababisha adha kubwa kwa wananchi wa maeneo hayo pamoja na upotevu wa ushuru. Mwaka 2016 aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi alitembelea mnada huo na kuagiza mnada ufunguliwe.
Je, ni kwa nini mnada huu wa Magena haujafunguliwa mpaka sasa ili kutoa fursa za ajira na kuokoa mapato yanayopotea?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, na mimi naomba uniruhusu kwanza kukukaribisha kama vile walivyokukaribisha Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika Bunge letu tukufu.
Mheshimiwa Spika, niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mnada wa Magena ulikuwa kati ya minada 10 ya mipakani uliokuwa chini ya Wizara ya Kilimo na Mifugo mwaka 1995. Mnada huo ulikamilika kujengwa mwaka 1995 na kufunguliwa mwaka 1996 ambapo ulifanya kazi kwa takriban mwaka mmoja, ambapo ng’ombe 104,000 waliuzwa na jumla ya shilingi milioni 260 zilikusanywa kama maduhuli ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza, ikiwemo wizi wa mifugo na sababu za kiusalama, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mara, tarehe 14 Mei, 1997 iliagiza mnada huo ufungwe na kuwapatia wafugaji mnada mbadala wa Mpakani. Kutokana na hali hiyo, uongozi wa Mkoa wa Mara uliiomba Wizara ya Maendeleo ya Mifugo ya wakati huu ifute mnada wa Magena na Kirumi Check Point iteuliwe kuwa mnada wa mpakani kwa kuwa tayari kuna kizuizi cha Mto Mara.
Mheshimiwa Spika, Wizara ilikubali ombi la uongozi wa Mkoa wa Mara na hivyo ikaanza kujenga mnada eneo la Kirumi sehemu ambayo kuna kizuizi cha asili cha Mto Mara na ujenzi huu umekamilika kwa asilimia 80 na unatarajiwa kufunguliwa mwaka huu wa 2017/2018. Kwa kuwa kazi ya Kituo cha Polisi inaendelea na kazi ya kuweka umeme katika eneo lile imekamilika.
Mheshimiwa Spika, mafanikio ya Mnada wa Kirumi yameanza kuonekana ambapo Wizara kwa kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Mara, kuanzia mwezi Julai, 2016 hadi Februari, 2018 imekusanya jumla ya shilingi 221,270,000 kutokana na vibali na faini mbalimbali za ng’ombe 9,842, mbuzi na kondoo 4,886 kutoka Mikoa ya Rukwa, Kagera, Simiyu, Shinyanga, Mara na Mwanza waliokuwa wakisafirishwa kwenda Kenya bila ya vibali. (Makofi)
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-
Je, ule mpango wa Serikali wa kuzalisha vifaranga na kuwapa wafugaji umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali wa kuzalisha na kusambaza vifaranga kwa wafugaji wa samaki unaendelea kutekelezwa kupitia bajeti ya kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imeendelea na mkakati wake wa kuimarisha miundombinu ya uzalishaji wa vifaranga bora vya samaki katika vituo vyake vya Kingolwira (Morogoro), Mwamapuli (Tabora) na Ruhila (Ruvuma) ambapo kwa kipindi cha mwaka 2009/2010 mpaka mwaka 2017/2018 jumla ya vifaranga milioni 21 vilizalishwa na kusambazwa kwa wafugaji kwa bei ya ruzuku ya shilingi 50 kwa kifaranga aina ya sato na shilingi 100 kwa kifaranga aina ya kambale.
Mheshimiwa Mwenekiti, aidha, bei ya vifaranga kwenye mashamba ya watu na taasisi binafsi ni kati ya shilingi 150 hadi shilingi 300 kwa kifaranga kimoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 Wizara imekamilisha ujenzi wa hatchery ya kisasa ya kituo cha Kingolwira (Morogoro) yenye vitotoleshi 20 vyenye uwezo wa kuzalisha vifaranga takribani milioni 15 kwa mwaka.
Aidha, ni mkakati wa Wizara kujenga hatchery kama hiyo na kufunga vitotoleshi kama hivyo kwenye vituo vya Mwamapuli (Tabora) na Ruhila (Ruvuma) kwa lengo la kuzalisha takribani vifaranga milioni 45 kwa mwaka kutoka sekta ya umma ifikapo mwaka 2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika kudhibiti ubora wa vifaranga wa samaki wa kufugwa Wizara imeendelea na mkakati wake wa kuimarisha vituo vyake kwa lengo la kuhifadhi samaki wazazi bora (broodstock) watakao sambaza kwenye hatchery za sekta binafsi zinazotambuliwa na Wizara ili kuongeza uzalishaji wa vifaranga kwa mwaka kutoka vifaranga 14,120,000 (2016/2017) hadi vifaranga 60,000,000 ifikapo mwaka 2022.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imeendelea kuhamasisha Halmashauri na sekta binafsi kuanzisha vituo vya kuzalisha vifaranga bora vya samaki ambapo vituo 23 vimeanzishwa na kuzalisha takribani vifaranga milioni 20 kwa mwaka na kusambazwa kwa wafugaji. Aidha, ni lengo la Wizara kushirikiana na mamlaka za Serikali za Mitaa na sekta binafsi kutekeleza mikakati wa kuongeza uzalishaji wa samaki wa kufuga kutoka tani 10,000 tulizonazo sasa hadi tani 50,000 ifikapo mwaka 2020/2021(Makofi).
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Kumekuwa na changamoto nyingi katika uvuvi wa Ziwa Victoria unaosababisha malalamiko mengi kutoka kwa wadau wa uvuvi.
Je, Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha inamaliza malalamiko hayo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uvuvi wa Ziwa Victoria umekuwa na changamoto nyingi zikiwemo shughuli za uvuvi haramu uliokithiri ambapo takribani asilimia 90 ya wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi hufanya vitendo vya uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo hivyo ni pamoja na kuvua kwa kutumia nyavu zilizounganishwa (vertical integration), kutumia nyavu za utali/timba (monofilament nets), kuvua kwa makokoro na nyavu zenye macho madogo chini ya kiwango kinachokubalika kisheria cha milimita nane na kadhalika. Aidha, uchakataji na biashara ya samaki wachanga na utoroshaji wa mazao ya uvuvi yakiwemo mabondo na kayobo kwenda nchi jirani bila kuzingatia sheria ni mojawapo ya vitendo vinavyoshawishi uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na vitendo hivyo, Serikali imedhamiria kulinda rasilimali za Taifa kwa kufanya Operesheni Sangara mwaka 2018 dhidi ya uvuvi haramu katika Ziwa Victoria. Operesheni hii ni kweli imeleta malalamiko kwa baadhi ya wadau wa uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kushughulikia malalamiko hayo, Serikali inaendelea kuhamasisha wavuvi, wafanyabiashara, watendaji wa Serikali na wadau wengine wote kufuata sheria na kanuni za uvuvi na kufanya mapitio ya Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 ili kuendana na mabadiliko ya sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imetoa elimu na inaendelea kutoa elimu kwa wadau wote kuhusu uvuvi endelevu. Pamoja na kufanya tafiti mbalimbali zinazosaidia wadau katika kuendeleza Sekta ya Uvuvi nchini katika kuchangia ukuaji wa uchumi wetu na wananchi wetu kwa ujumla. Tafiti hizo zinalenga kufanyika katika samaki wa maji ya asili na ukuzaji viumbe katika maji (aquaculture).
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kufanya tafiti zitakazopendekeza zana na njia sahihi za uvuvi zisizo na ahari katika uvunaji wa rasilimali za uvuvi. Pia kuimarisha vikundi vya ulinzi shirikishi wa rasilimali za uvuvi na kuandaa mwongozo wa kuvifanya vikundi hivyo kufanya kazi zake kwa ufanisi ili kutokomeza uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inatarajia kufanya semina kwa Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania kwa lengo la kutoa uelewa mpana kuhusu uvuvi haramu na jitihada zinazofanywa na Wizara yetu kupambana na uvuvi haramu kupitia operesheni zinazofanyika zikiwemo Operesheni Sangara, Jodari na ile ya MATT.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Mwaka 1974 Tanzania iliridhia Mkataba wa Kuzuia Uchafuzi wa Bahari na Usalama wa Bahari ambao lengo mojawapo ni kuzuia uvuvi haramu wa kutumia mabomu na kutoa misaada ya vifaa vya kuzuia uchafuzi wa bahari:-
(a) Je, Serikali imeweka mikakati gani ya kuzuia uvuvi haramu wa kutumia mabomu ambao bado unaendelea?
(b) Je, Serikali inawasaidiaje wavuvi ili waachane na uvuvi haramu wa kutumia mabomu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mikakati mbalimbali ya kupambana na uvuvi haramu ukiwemo uvuvi wa kutumia mabomu, mikakati hiyo ni pamoja na:-
(a) Kuimarisha ushirikishwaji wa jamii katika kusimamia na kulinda rasilimali za uvuvi kupitia Halmashauri, Serikali za Vijiji na Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi kwa maana ya BMUs;

(b) Kuendelea kutoa elimu kuhusu athari za uvuvi haramu kwa mazingira, jamii na uchumi;
(c) Kufanya maboresho ya sheria ili kuwa na sheria kali dhidi ya uvuvi haramu hasa uvuvi wa kutumia mabomu ama milipuko ikiwa ni pamoja na kuweka kipengele cha kuonesha uvuvi haramu ni uhujumu wa uchumi; na
(d) Kuimarisha Mashirikiano ya Kikanda na Kimataifa kwa kushirikiana na nchi mbalimbali zikiwemo nchi za SADC katika kuzuia uvuvi usioratibiwa na usioripotiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inaendelea kufanya operesheni ikiwa ni pamoja na Operesheni Sangara, Jodari na operesheni za Kikosi cha Kitaifa kwa maana ya Mult Agency Task Team (Matt) cha kuzuia uharibifu wa mazingira ili kulinda rasilimali za uvuvi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia MATT, Serikali imefanya operesheni katika Mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani, Tanga na Dar es Salaam ambapo mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na kupungua kwa idadi ya milipuko kutoka asilimia 88 kwa mwezi hadi kufikia asilimia mbili mwezi Machi 2018, kukamatwa kwa vifaa vya milipuko na watuhumiwa 32 ambapo kesi 13 zimefunguliwa mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuwasaidia wavuvi kuachana na uvuvi haramu ukiwemo wa kutumia mabomu, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wavuvi wa jamii za Ukanda wa Pwani kuhusu athari za uvuvi haramu kama vile uharibifu wa mazingira, matumbawe, mazalia na makulio ya samaki, kusababisha jangwa katika bahari, kuua viumbe vingine visivyo kusudiwa, vifo, ulemavu ili waache kabisa vitendo hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inaendelea kuwahimiza wavuvi kujiunga katika vikundi na kuanzisha Vyama vya Ushirika vya Msingi, Vyama vya Akiba kwa maana ya SACCOS na VICOBA ili waweze kukopesheka na kuweza kununua zana na vyombo bora vya uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefuta Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye injini za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu pamoja na nyuzi kwa ajili ya nyavu za uvuvi na vifungashio kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2011na Sheria ya Mamlaka ya Mapato (VAT) ili kuwasaidia wavuvi kupata zana za uvuvi kwa bei nafuu. Aidha, Serikali inahamasisha sekta binafsi kujenga viwanda vya kutengeza boti na zana bora za uvuvi ili kuwezesha wavuvi kuzipata kwa bei nafuu na kwa urahisi.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA aliuliza:-
Wilaya ya Ulanga ina ongezeko la mifugo; ng’ombe, mbuzi, kondoo na nguruwe lakini hakuna huduma za mifugo kama vile majosho:-
Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa majosho?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Goodluck Mlinga, Mbunge wa Ulanga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inafahamu ongezeko la mifugo katika wilaya mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Ulanga inayokadiriwa kuwa na idadi ya mifugo kama ifuatavyo: Ng’ombe 70,000; mbuzi 16,000 na kondoo 6,373.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imepokea ombi la Mheshimiwa Goodluck Mlinga na kwa kushirikiana na wadau wengine litazingatiwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-
Ni Sera ya Taifa kuwawezesha Wavuvi ili wafanye shughuli zao kwa tija:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha Wavuvi katika Ukanda wa Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ili kuwawezesha wavuvi hususan kununua vifaa kwa bei nafuu, Serikali imeondoa kodi ya ongezeko la thamani yaani VAT kwa engine za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu, vifungashio na nyavu zenyewe. Pia kulingana na chapisho la Afrika Mashariki kuhusu ushuru wa pamoja la mwaka 2007 - 2012, engine za uvuvi, malighafi zinazotumika kutengeneza zana mbalimbali za uvuvi na viambata vyake vinavyonunuliwa katika Soko la Afrika Mashariki hupewa punguzo la kodi ama kufutiwa kodi kabisa.
Mheshimiwa Spika, hatua hii itasaidia kupungua kwa bei za zana za uvuvi ambapo wavuvi wataweza kunufaika na mpango huo hatimaye kumudu kununua zana za uvuvi.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeanzisha Benki ya Kilimo ambayo inatoa fursa kwa wavuvi kupata mikopo kwa ajili ya kununua zana za uvuvi. Aidha, Serikali inaendelea kuwahamasisha wavuvi kujiunga kwenye Mifuko ya huduma za kijamii ikiwemo Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, kama vile NSSF ambapo Mfuko wa NSSF umeanzisha utaratibu unaojulikana kama Wavuvi Scheme ili kuwawezesha wavuvi kupata huduma za kijamii zinazotolewa na mfuko huu kama vile huduma za afya pamoja na kupewa malipo ya uzeeni.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na operesheni ya kudhibiti uvuvi haramu na biashara ya haramu ya mazao ya samaki inayokwenda kwa jina la Operesheni Sangara. Operesheni hii inalenga katika kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinalindwa ili ziweze kuwasaidia wananchi na Taifa kwa ujumla katika kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja na kuongeza Pato la Taifa. Pia inalenga katika kutunza rasilimali na mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
MHE. MARY D. MURO aliuliza:-
Shamba la Vikuge lilikuwa mkombozi kwa wananchi wa Kibaha na Dar es Salaam kujipatia majani ya kulisha mifugo yao, lakini kwa sasa shamba hilo limegeuka pori. Je, Serikali ina kauli gani kuhusu shamba hilo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI nlijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba la kuzalisha mbegu bora za malisho la Vikuge - Kibaha, ni moja wapo kati ya mashamba saba ya Wizara yanayozalisha mbegu bora za malisho. Mbegu hizo huuzwa kwa wafugaji na wadau wengine ili kuwekeza katika uzalishaji wa malisho kwa ajili ya kuwa na ufugaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili pia huzalisha hei na kuwauzia wafugaji wa Kibaha, Dar es Salaam na kwingineko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba lina ukubwa wa jumla ya hekta 515 ambapo eneo la hekta 30 ni makazi, hekta 20 ni hifadhi ya vyanzo vya maji na eneo linaloendelezwa ni hekta 250. Eneo lililobaki si pori bali ni eneo la akiba lenye malisho ya asilia ambalo huwa linafyekwa vichaka na kuvunwa malisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa 2017/2018 shamba la Vikuge limezalisha jumla ya marobota ya hei 26,000 na mbegu bora za malisho kilo 1,500 ambazo zinauzwa kwa wadau wa malisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shamba la Vikuge katika mwaka wa 2018/2019 Serikali imejipanga kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za malisho na hei kwa kuendeleza eneo jipya la hekta 20.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Jimbo la Mlimba lina mito mingi inayotiririka mwaka mzima ambayo inaweza kutumika kujenga malambo kwa ajili ya mifugo:-
Je, ni lini Serikali itajenga Malambo kwa ajili ya kunyweshea mifugo katika Jimbo la Mlimba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, kama ifauatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba uwepo wa mito mingi katika Jimbo la Mlimba ni fursa kwa ajili ya upatikanaji wa maji kwa matumizi mbalimbali ikiwemo mifugo.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Wizara yangu imepokea ombi la Mheshimiwa Susan Kiwanga na litazingatiwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019. Pia nitoe wito kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuendelea kuhamasisha sekta binafsi, wafugaji pamoja na wadau wa maendeleo kuibua miradi ya ujenzi wa malambo, mabwawa, majosho na visima virefu kwa lengo la kuboresha shughuli za ufugaji ili kuleta tija.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
Mradi wa machinjio ya kisasa wa Ngerewara uliopo Manispaa ya Iringa umekuwa ni wa muda mrefu sana toka umeanza.
Je, ni lini Serikali italeta fedha za kutosha ili kumaliza mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa machinjio ya kisasa wa Ngerewara unatekelezwa na Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kwa kushirikiana na wadau wengine. Mradi ulianza kutekelezwa mwaka 2008/2009 na ulikadiriwa kugharimu shilingi za Kitanzania 1,900,000,000. Aidha, mpaka sasa kiasi cha shilingi 928,000,000 zimetumika kugharamia mradi huu kupitia Serikali Kuu, Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, Mradi wa ASDP na Shirika la Maendeleo la Viwanda la Umoja wa Mataifa ambalo lilisaidia kuweka vifaa vya machinjio vikiwemo mashine za kuchakata nyama na vyumba viwili vya kuhifadhi ubaridi (cold rooms).
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa sehemu kubwa ya miundombinu inayohitajika kwa ajili ya machinjio imekamilika. Aidha, kiasi cha shilingi 1,090,000,000 zinahitajika kwa ajili ya kugharamia ujenzi wa zizi, mabwawa matatu ya maji machafu na maji safi, uzio wa machinjio, tanuru la kuchomea taka kwa maana ya incinerator, jengo la ofisi za utawala, vyoo, jiko na kisima cha maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara itashirikiana na Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kuhakikisha fedha za kukamilisha machinjio ya Ngerewara zinapatikana ili Watanzania wapate ajira na bidhaa abora za mifugo na kuongeza pato la Halmashauri na Taifa kwa ujumla wake.
MHE. ALLY S. UGANDO (K.n.y. MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA) aliuliza:-
Wananchi wa Kata za Mwaseni, Mloka, Ngoroko na Kipungila Wilayani Rufiji waliruhusiwa kuingia ndani ya Hifadhi ya Selous na kuvua samaki na hivyo kuinuka kiuchumi. Baada ya marekebisho ya mipaka ya hifadhi wamezuiwa kuingia kwenye hifadhi na wakati mwingine wanatendewa vitendo kinyume na sheria.
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani kusaidia wananchi wa maeneo hayo ili waweze kupata kipato?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani kurejesha amani kati ya vijiji vinavyozunguka maeneo ya mipaka ya hifadhi na watumishi wa hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka 1990 Pori la Akiba la Selous lilianzisha Mpango wa Ushirikishwaji Jamii zinazozunguka pori hilo katika uhifadhi chini ya mradi ulioitwa Selous Conservation Programme (SCP). Katika kutekeleza mpango huo, wananchi wa jirani waliruhusiwa kuvua samaki ndani ya Pori la Akiba la Selous kwa ajili ya kitoweo baada ya kuombwa na wananchi wa Vijiji vya Kata za Mwaseni na Ngorongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kibali hicho kilisitishwa baada ya kuwepo ukiukwaji wa masharti yaliyotolewa ambapo baadhi ya wanavijiji waliingia ndani ya hifadhi bila kujisajili au kujiandikisha na kuvua samaki kwa ajili ya kufanya biashara kinyume na kusudio la kibali hicho. Aidha, baadhi ya wanavijiji walitumia fursa hiyo kufanya ujangili ndani ya pori kwa kuingia na silaha walizoficha ndani ya mitumbwi yao na kuua tembo, faru na wanyamapori wengine. Kutokana na sababu hizi, Serikali haina mpango wa kuruhusu uvuvi katika Pori la Akiba Selous. Nashauri Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na Serikali kuelimisha wananchi kuvua katika mabwawa yaliyo nje ya hifadhi pamoja na kuhamasisha ufugaji wa samaki kibiashara ili kujipatia kitoweo na kipato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kuimarisha mahusiano mema kati ya wahifadhi na jamii inayozunguka maeneo yanayohifadhiwa itaendelea kuhakikisha inatoa elimu kwa jamii na kushirikiana nayo kwenye shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
MHE. AMINA N. MAKILAGI aliuliza:-
Wavuvi wadogowadogo hawana teknolojia rafiki inayowawezesha kuvua kwenye maeneo yenye samaki wengi:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha maeneo ya uvuvi kwa kutumia teknolojia rafiki kuweka vifaa vya kuvulia samaki (Fish Aggregating Devices) ili kuongeza upatikanaji wa samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassoro Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) imeandaa programu ya kuweka vifaa maalum vya kuvutia samaki (Fish Aggregating Devices – FADs) kwenye bahari kwa kushirikiana na wavuvi. Kwa kuanzia programu hii inatekelezwa katika Wilaya ya Bagamoyo kwa upande wa Tanzania Bara na Nungwi, Tanzania Visiwani, ambapo vikundi viwili vya wavuvi kila upande vinafundishwa jinsi ya kutengeneza FADs na kuziweka baharini ili kuwasaidia wavuvi kupata samaki wengi na kutumia muda mfupi katika kuvua.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu inafadhili programu hii ambapo jumla ya FADs 70 zimekwishatengenezwa na kuwekwa baharini katika maeneo ya Bagamoyo, Mafia na Visiwa vya Unguja na Pemba. Vilevile, wavuvi wameweka FADs za asili ambazo hutengenezwa kwa kutumia magogo ya minazi na magari chakavu katika maeneo ya Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo. Aidha, Serikali inaandaa mpango wa kufuatilia upatikanaji wa samaki baada ya FADs hizo kuwekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itahakikisha programu hii inafanikiwa na teknolojia hii inasambazwa katika maeneo mengine ili wavuvi waweze kufaidika.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS (K.n.y. MWANTAKAJE HAJI JUMA) aliuliza:-
(a) Je, ni lini Serikali itawapatia mtaji na kuwawezesha kiuchumi wananchi wengi ambao wamejiunga katika vikundi vya uvuvi?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia vifaa vya kisasa ili kuondokana na vifaa haramu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Bububu, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeweka mazingira mazuri kwa wavuvi kupata mikopo ya masharti na riba nafuu kutoka katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo na kupitia Dirisha la Kilimo katika Benki ya Rasilimali. Mikopo hiyo itawezesha wavuvi kununua zana bora za uvuvi. Pia, Serikali inaendelea kuwahimiza wavuvi kujiunga katika vikundi na kuanzisha Vyama vya Ushirika vya Msingi, Vyama vya Akiba na Mikopo (SACCOS) na VICOBA ili waweze kukopesheka na kuweza kununua zana na vyombo bora vya uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hairuhusu matumizi ya vifaa haramu kwenye uvuvi kwa mtu yeyote kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 na sheria nyingine za nchi. Aidha, Serikali imefuta Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye injini za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu, nyavu za uvuvi na vifungashio kwa kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2011 na Sheria ya Mamlaka ya Mapato ili kuwasaidia wavuvi kupata zana za uvuvi kwa bei nafuu. Pia, Serikali inaendelea kuwahamasisha wavuvi kujiunga kwenye Mifuko ya Huduma za Kijamii ukiwemo Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ambao umeanzisha utaratibu unaojulikana kam Wavuvi Scheme ili kuwawezesha wavuvi kupata huduma za kijamii zinazotolewa na mfuko huu, kama vile huduma za afya pamoja na kupewa malipo ya uzeeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa ruzuku kwenye injini za kupachika ambapo Kikundi/Chama cha Ushirika cha Wavuvi kinatakiwa kuchangia asilimia 60 na Serikali asilimia 40 ya gharama. Aidha, Serikali inahamasisha sekta binafsi kujenga viwanda vya kutengeneza boti na zana bora za uvuvi ili kuwezesha wavuvi kuzipata kwa bei nafuu na kwa urahisi. (Makofi)
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Uvuvi wa Bahari Kuu unaingiza kipato kikubwa sana na unaweza ukachangia katika bajeti ya nchi yetu:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kununua meli za uvuvi?
(b) Je, Serikali imefikia wapi katika ujenzi wa Bandari ya Uvuvi nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo, lenye vipengele (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 - 2020 inaelekeza Serikali umuhimu wa nchi kuvuna rasilimali za uvuvi zilizopo katika ukanda wa Bahari Kuu kwa kuwa na meli za Kitanzania. Lengo la kununua meli hizo ni kuwa na meli za Kitaifa kuwezesha uvunaji wa rasilimali za uvuvi katika ukanda wa Bahari Kuu kwa lengo la kupata chakula na lishe, kuongeza Pato la Taifa na kutoa ajira kwa Watanzania watakaofanya kazi katika meli hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanikisha azma hiyo Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza utaratibu wa kufufua lililokuwa Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) hatua itakayowezesha meli zitakazonunuliwa kuwa chini ya usimamizi wa TAFICO. Makadirio ya kufufua Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ni jumla ya shilingi za Kitanzania bilioni 45 ikiwemo maandalizi ya ununuzi wa meli za uvuvi. Aidha, Wizara inahamasisha Mifuko ya Kijamii, Taasisi, Mashirika ya Umma na Watanzania kuwekeza katika uvuvi wa Bahari Kuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara tayari imempata mtaalam mwelekezi atayefanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ambapo kukamilika kwa kazi hii kutawezesha kujua gharama halisi za ujenzi na aina na ukubwa wa bandari itakayojengwa. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza:-
Tatizo la uvuvi haramu bado linaendelea licha ya jitihada za Serikali kuchoma nyavu za uvuvi zisizopendekezwa:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kukomesha uvuvi haramu zaidi ya kuchukua hatua hiyo ya kuchoma nyavu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara imepewa jukumu la kulinda, kusimamia, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za uvuvi nchini kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009. Katika kutekeleza jukumu hili, Serikali imekuwa ikifanya jitihada kudhibiti vitendo vya uvuvi haramu kwa kufanya doria za mara kwa mara pamoja na kufanya operesheni mbalimbali ikiwemo Operesheni Sangara ya mwaka huu wa 2018, Operesheni Jodari na za Kikosi Kazi cha Kitaifa, kwa maana ya Mult (Multi-Agency Task Team - MATT) cha kuzuia uharibifu wa mazingira ili kulinda rasilimali za uvuvi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Spika, Serikali inayo mikakati mbalimbali ya kupambana na uvuvi haramu. Mikakati hiyo ni pamoja na: Kuimarisha ushirikishwaji wa jamii katika kusimamia na kulinda rasilimali za uvuvi kupitia halmashauri, Serikali za Vijiji na Vikundi vya Usimamizi Shirikishi (BMU’s); kuendelea kutoa elimu kuhusu athari za uvuvi haramu kwa mazingira, jamii na kiuchumi; kufanya maboresho ya sheria ili kuwa na sheria kali dhidi ya uvuvi haramu hasa uvuvi wa kutumia mabomu/ milipuko, ikiwa ni pamoja na kuweka kipengele cha kuonesha uvuvi haramu ni sawa na uhujumu uchumi; na kuimarisha Mashirikiano ya Kikanda na Kimataifa kwa kushirikiana na nchi mbalimbali zikiwemo nchi za SADC katika kuzuia uvuvi uisoratibiwa na usioripotiwa.
Mheshimiwa Spika, Wizara inahamasisha ufugaji wa samaki ili kupunguza nguvu ya uvuvi kwenye maji ya asili. Aidha, naomba Waheshimiwa Wabunge wote watusaidie katika kuwaelimisha wananchi kuachana na vitendo vya uvuvi haramu na kushiriki katika kulinda rasilimali za nchi yetu. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-
(a) Je, ni utafiti gani umefanyika katika Ziwa Victoria mpaka kufikia hatua ya kuzuia uvuvi wa aina yoyote kwa kisingizio cha uvuvi haramu?
(b) Je, ni sheria gani inatumika kukamata nyavu na ndani ya dakika kumi zinachanwa bila ya kumpa mvuvi nafasi ya kujitetea?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali haijazuia uvuvi wa aina zote kufanyika katika Ziwa Viktoria. Uvuvi unafanyika nchini kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 pamoja na sheria nyingine za nchi yetu. Aidha, kwa sasa Serikali inapambana na uvuvi haramu katika Ziwa Viktoria kama ilivyo katika maeneo mengine kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za uvuvi hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, upo utaratibu wa kisheria wa kukamata na kuharibu zana za uvuvi zinazotumika katika uvuvi haramu. Taratibu hizo zimeelezwa vizuri kwenye Kanuni Na. 50(1), (2) na (5) ya Kanuni za Uvuvi za mwaka 2009. Aidha, nyavu haramu huteketezwa kwa idhini ya Mahakama baada ya taratibu zote za kisheria kufuatwa.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y. MHE. JANETH M. MASSABURI) aliuliza:-
Je, Serikali haioni kuwa kusuasua kwa Chuo cha Uvuvi Mbegani - Bagamoyo na vyuo vingine kutokana na kukosa bajeti ya kutosha ya kuviendesha vyuo hivyo kumechangia kupoteza ajira kwa vijana ambao kama wangepata mafunzo ya ufugaji samaki wangeinuka kimapato?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janeth Maurice Massaburi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Janeth Maurice Massaburi kwa kuwa ni kiongozi wa mfano kwa ufuatiliaji na kitendo chake cha kuwalipia watoto wake wawili kupata mafunzo ya ufugaji wa samaki katika Chuo cha Mbegani kwa muda wa wiki moja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuimarisha mafunzo ya uvuvi kwa kuanzisha Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) mwaka 2012 ambapo udahili umeongezeka kutoka wanafunzi 714 mwaka 2011/2012 hadi kufikia wanafunzi 1,196 katika mwaka wa 2016/2017. Pia, FETA imekuwa ikipokea fedha kutoka Serikalini ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018 ilipatiwa jumla ya shilingi milioni 246 kwa matumizi ya kawaida, katika mwaka huu wa fedha wametengewa shilingi milioni 580 kiasi ambacho ni zaidi ya mara mbili ya kile walichokipata katika mwaka uliopita.
Mheshimiwa Spika, kazi kubwa ya maendeleo iliyofanyika katika kipindi hiki cha miaka sita ya uhai wa FETA ni pamoja na kukarabati miundombinu ya vituo vya Mikindani - Mtwara, Kibirizi - Kigoma, Mwanza South pale Mwanza na Gabimori – Rorya. Vituo vya Mwanza South na Kibirizi tayari vimeanza kutumika kutoa mafunzo ya ufugaji wa samaki wakati vile vya Mikindani na Gabimori viko tayari kuanza kazi ya utoaji wa mafunzo na Serikali kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma tayari imekwishafanya kazi ya zoezi la usaili ili kupata wakufunzi 18 watakaopelekwa katika vituo hivyo ili kuviwezesha kuanza kazi katika mwaka huu wa fedha wa 2018/2019.
Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya mazungumzo na Jumuiya ya Ulaya (EU) ambayo imekubali kusaidia Wakala wetu hii FETA katika kujenga uwezo wa kitaasisi ili kupanua mafunzo ya kiufundi yanayolenga kuongeza idadi ya vijana watakaojiajiri ama kuajiriwa katika sekta ya ufugaji samaki. Utekelezaji wa mradi huu unaanza katika mwaka huu wa fedha 2018/2019 kwa kuandaa mitaala, miundombinu ya kufundishia na kujifunzia pamoja na kuwajengea uwezo wakufunzi wetu.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-
Halmashauri ya Makete ni miongoni mwa Halmashauri zinazozalisha maziwa ya ng’ombe kwa wingi:-
Je, ni lini Serikali itajenga Kiwanda cha Kusindika Maziwa katika shamba la Ng’ombe la Kitulo Makete - Njombe?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Shamba la Mifugo la Kitulo linalomilikiwa na Serikali lipo Wilaya ya Makete, Mkoa wa Njombe na lina mifugo kwa maana ya ng’ombe wa kisasa wapatao 799. Ng’ombe walioko Kitulo utumika kuzalisha mitamba pamoja na maziwa.
Mheshimiwa Spika, Wizara ina mpango wa kuboresha Shamba la Mifugo la Kitulo kwa kuboresha kosaafu za ng’ombe kwa kununua ng’ombe bora wa maziwa aina ya Holstein Friesian majike 400; kuongeza ng’ombe bora wa maziwa kutoka 450 waliopo hadi kufikia ng’ombe bora wa maziwa 1,200; kuongeza uzalishaji mitamba ya kuuza kutoka mitamba 80 kwa mwaka hadi mitamba 213 kwa mwaka; na kuongeza uzalishaji wa maziwa kutoka lita 400,000 kwa mwaka hadi lita 3,350,816 kwa mwaka ifikapo mwaka 2023.
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Njombe una Kiwanda cha Kusindika Maziwa cha Njombe Milk Factory, wakati Mkoa wa jirani wa Iringa una viwanda vya ASAS Dairy na Mafinga Milk Group ambapo kwa pamoja viwanda hivi vina uwezo wa kusindika lita 56,600 za maziwa kwa siku lakini vinasindika lita 18,300 tu kwa siku. Hivyo, wananchi wa mikoa hii wanayo fursa kubwa ya kuongeza uzalishaji wa maziwa ili kuwezesha viwanda hivyo kusindika kulingana na uwezo wa viwanda hivi.
Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya uanzishwaji wa viwanda ikiwemo kuboresha miundombinu ya barabara; kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika; kuondoa kodi kwenye mitambo na vifaa vya kupoozesha na kusafirishia maziwa; pamoja na kuhamasisha viwanda hivi kununua magari maalum ya kusafirisha maziwa ili viweze kufikia wafugaji katika maeneo yao.
MHE. ZAYNAB M. VULU aliuliza:-
Kilimo cha mwani kinalimwa baharini na asilimia kubwa ya wakulima wa zao hilo ni wanawake:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha zao hilo?
(b) Je, Serikali inamsaidiaje mkulima wa mwani kupata soko la uhakika hususani nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaynab Matitu Vulu, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, kilimo cha zao la mwani kinachofanyika katika mwambao wa Bahari ya Hindi ni miongoni mwa shughuli za sekta ndogo ya ukuzaji wa viumbe kwenye maji ambapo jumla ya tani 1,197 zenye thamani ya shilingi milioni 412 zilivunwa na kusafirishwa nje ya nchi mwaka 2016/2017. Aidha, tani 1,329 zenye thamani ya shilingi milioni 469 zilivunwa mwaka 2017/2018. Mwani hulimwa zaidi na wanawake wanaokadiriwa kuwa asilimia 90 ya wakulima.
Mheshimiwa Spika, mwaka 2005 Serikali iliandaa Mpango Madhubuti wa Maendeleo ya Mwani kwa lengo la kukabiliana na changamoto za kilimo cha mwani zikiwemo kiasi kidogo cha mwani kinachozwalishwa na wakulima pamoja na mapato duni. Malengo mahsusi ya Mpango Madhubuti wa Maendeleo ya Mwani ni pamoja na kujenga uwezo wa wakulima kujitegemea; kuongeza mwamko juu ya kilimo cha mwani kama shughuli inayozalisha mapato mazuri; na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji ambayo yanachochea uwekezaji wa kisasa na kudumisha matumaini ya wadau wote wa tasnia ya mwani.
(b) Mheshimiwa Spika, mwani unaozalishwa nchini unauzwa katika masoko ya nchi za Ufilipino, Uchina, Ufaransa na Denmark. Pia kiasi kidogo cha mwani husindikwa hapa nchini na wadau kwa kutengeneza sabuni za mche, sabuni za maji na shampoo. Pia, mwani husindikwa ajili ya chakula na dawa.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaongeza kasi ya utekelezaji wa Mpango Madhubuti wa Maendeleo ya Mwani ikiwa ni pamoja na kuongeza uzalishaji; kusaidia wananchi kuingia mikataba yenye tija na makampuni ya mwani; pamoja na kutafuta masoko mapya ya nje ili kusaidia wakulima kupata bei bora zaidi.
MHE. SILYVESTRY F. KOKA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha bidhaa za nyama nchini pamoja na mazao mengine yatokanayo na mifugo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugona Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sylvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inatekeleza mpango mkakati wa kuendeleza sekta ya mifugo ambao unelanga katika kupunguza umasikini na kuboresha mazingira rafiki na endelevu katika uzalishaji wa mifugo yenye tija kwa kuzalisha mitamba milioni moja kwa mwaka kutokana na makundi ya ng’ombe wa asili kwa kufanya uhimilishaji, kuimarisha upatikanaji wa uhakika wa maji, malisho na vyakula bora vya mifugo, kuhamaisha matumizi ya teknolijia za ufugaji wa kisasa, kuboresha afya, masoko, biashara na uongezaji wa thamani wa mazao ya mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara inatekeleza mkakati wa kudhibiti magonjwa ya mifugo na matumizi ya dawa, chanjo na viwatilifu vya mifugo nchini ambapo inatarajiwa kupunguza vifo vya mifugo kwa zaidi ya asilimia 80 pamoja na kuwa na mifugo bora kwa ajili ya masoko ya ndani na nje kwa ajili ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mkakati huu unatarajiwa kuwa na matokeo yafuatayo; kuongezeka kwa ukuaji wa sekta ya mifugo kutoka asilimia 2.8 hadi asilimia 5.2; kuongezeka kwa mchango wa sekta ya mifugo katika pato la Taifa kutoka asilimia 6.9 hadi asilimia 9; kuongeza uzalishaji wa mazao ya mifugo kama vile kuongeza idadi ya ng’ombe wa maziwa 789,000 ambao tulionao hii leo hadi kufikia ng’ombe wa maziwa milioni tatu; kuongeza uzalishaji wa maziwa kutoka lita bilioni 2.4 hadi kufikia lita bilioni 3.8 kwa mwaka; kuongeza uzalishaji wa nyama kutoka tani 679,992 hadi tani 882,100; kuongeza uzalishaji wa ngozi kutoka futi za mraba milioni 89 hadi kufikia futi za mraba milioni 98.9 na kuongeza uzalishaji wa mayai bilioni 3.2 hadi bilioni 6.4. Pia mkakati unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za ugani, kuongeza uzalishaji wa chanjo za mifugo zinazozalishwa hapa nchini, kupongeza usindikaji wa mazao na mifugo pamoja na kuongeza usambazaji wa teknolojia za ufugaji bora ili kufikia wafugaji wengi zaidi.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:-
(a) Je, Ranchi ya Missenyi ina ng’ombe wangapi kwa sasa?
(b) Je, wananchi wanaoizunguka ranchi hiyo wananufaikaje kutokana na uwepo wake?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI aliuliza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Diodorus Buberwa Kamala, Mbunge wa Nkenge lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ranchi ya Missenyi iliyopo Wilayani Missenyi, Mkoani Kagera ni miongoni mwa ranchi sita za mfano zinazoendeshwa na Kampuni ya Taifa ya Ranchi (NARCO). Ranchi hii kwa sasa ina ng’ombe 1,670, mbuzi 212 na kondoo 120. NARCO inaendelea kuiboresha na kuiongezea mifugo zaidi ili iweze kwenda sambamba na eneo lake ambalo ni hekta 23,998.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ranchi ya Missenyi hutumika kama shamba darasa kwa jamii ya wafugaji na inatoa elimu ya nadharia na vitendo kwa wafugaji kuhusu ufugaji wenye tija. Vilevile ranchi hii hutoa fursa ya upatikanaji wa mifugo bora kwa ajili ya nyama na uzalishaji mitamba chotara kwa ajili ya wafugaji wa ng’ombe wa maziwa. Katika kipindi cha mwaka 2017/2018 jumla ya mitamba 12 iliuzwa kwa wafugaji wa ng’ombe wa maziwa katika Kata ya Mabale na mbuzi sita walitolewa na ranchi kwa wafugaji wa Kitongoji cha Rwengiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2018/2019 NARCO imepanga kutenga vitalu kwenye baadhi ya ranchi zake ikiwemo Ranchi ya Missenyi kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji wa maeneo ya jirani kupata maeneo ya malisho na maji wakati wa kiangazi.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM aliuliza:-
Wavuvi wengi nchini wanaendesha shughuli zao za uvuvi kwa kutumia njia zisizokuwa za kitaalam.
Je, ni lini Serikali itatoa mafunzo ya kitaalam kwa wavuvi wetu ili kuwawezesha kufanya kazi yao kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Salim Maalim, Mbunge wa Kojani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) imefanya na inaendelea kufanya tafiti zitakazosaidia wavuvi kutumia njia za kitaalam katika uvuvi kwa lengo la kuboresha uvuvi na mapato ya wavuvi. TAFIRI inao mradi wa kuyatambua maeneo yenye samaki kwa maana (Potential Fishing Zones - PFZs) katika Bahari ya Hindi ili kuwasaidia wavuvi kutumia muda mfupi na rasilimali chache kuyafikia maeneo hayo na hivyo kuboresha mavuno ambayo yataongeza pato la mvuvi na Taifa kwa ujumla. Wavuvi wanapewa taarifa za kijiografia kupitia GPS, kupitia simu zao za mkononi kujua maeneo yenye samaki kwa msimu husika. Mradi huu kwa sasa ni wa majaribio na unafanyika kwa kushirikiana na wavuvi wa maeneo ya Mafia na Tanga kwa Tanzania Bara na pia Unguja na Pemba kwa Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara pia kupitia Taasisi yetu ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) inaendelea na mradi wa vikusanya samaki yaani Fish Aggregating Devises-FADs katika Bahari ya Hindi ambapo inashirikiana na wavuvi wa Bagamoyo kwa upande wa (Tanzania Bara) na Nungwi kwa upande wa Tanzania Visiwani ambapo lengo kubwa la mradi ni kuwasaidia wavuvi waweze kwenda kuvua sehemu zilizo na samaki na kuachana na uvuvi wa kuwinda ambao unapoteza muda na rasilimali.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-
Asilimia 95 ya eneo lote la Wilaya ya Longido hutumika kwa ufugaji wa wanyamapori. Aidha, asilimia tano ya eneo hilo ndiyo hutumika kwa shughuli za kilimo.
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuendeleza sekta ya mifugo kwa kuzingatia kuwa mifugo ndio shughuli kuu ya uchumi wa wananchi wa Longido na Wilaya nyingine za ufugaji nchini?
(b) Je, ni lini Serikali itapatia Hati ya Idhini ya kutumia na kusimamia (User Rights Certificate) Jumuiya ya Uhifadhi wa Wanyama Pori (WMA) wa Kanda ya Lake Natron?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mbunge wa Longido lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imeandaa mkakati wa kuboresha sekta ya mifugo nchini unaolenga kuongeza tija na uwekezaji katika mifugo, kuboresha mfumo wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali yatokanayo na biashara ya mifugo na mazao yake ili kuongeza mchango wa mifugo katika Pato la Taifa. Aidha, mikakati ya kuendeleza sekta ya mifugo katika Wilaya ya Longido inahusisha ujenzi wa mnada wa kimkakati wa Eworendeke ambao umekamilika na unatarajiwa kuzinduliwa rasmi Julai, 2018. Mnada huu utasaidia wafugaji kupata soko la uhakika la mifugo. Pia, Halmashauri ya Longido imepata mwekezaji ambaye atajenga kiwanda cha kusindika nyama katika eneo la Eworendeke ambacho kinatarajiwa kukamilika mwezi Disemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Wilaya ya Longido kuwa na Hali ya Ukame Halmashauri imejenga mabwawa, vibanio vya kunyweshea mifugo pamoja na kusambaza madume bora ya ng’ombe kwa lengo la kuboresha mifugo ya asili ilikupata mifugo bora inayostahimili mazingira ya Longido na kukua kwa haraka. Pia Halmashauri itaendelea kutoa huduma za ugani kwa wafugaji kwa lengo la kuboresha ufugaji ikiwamo kutoa mafunzo kuhusu mabadiliko ya tabia ya nchi na uboreshaji wa maeneo ya malisho.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Ziwa Natron ni pori tengefu kwa mujibu wa Kanuni za Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) za mwaka 2012 kifungu cha 8(1)(a)- (c). Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori huanzishwa katika maeneo yaliyo nje ya maeneo yaliyohifadhiwa kisheria. Aidha, hati ya matumizi ya rasilimali za wanyama pori kwa maana ya User Rights Certificate hutolewa kwa Jumuiya ya Hifadhi za Wanyama pori iliyoanzishwa na kusajiliwa kisheria. Kwa kuwa eneo hilo bado ni Pori Tengefu, limeendelea kupangiwa vitalu vya uwindaji wa kitalii ambapo wananchi na Halmashauri ya Wilaya wananufaika na asilimia 25 ya mapato yatokanayo na ada za wanyamapori wanaowinda.
MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-
Busokelo ni miongoni mwa Halmashauri zinazozalisha maziwa ya ng’ombe kwa wingi ambapo kwa mwaka inazalisha zaidi ya lita milioni 50:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kumalizia Kiwanda cha Maziwa kinachojengwa Kata ya Isange ili kunusuru maziwa mengi yanayoharibika kwa kukosa soko?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Maziwa cha Isange kilianza kujengwa na Serikali mnamo mwaka 2012 chini ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Kwanza (Agricultural Sector Development Programme – ASDP – Phase I). Kupitia programu hiyo shilingi milioni 140 zilitolewa na kutumika kujenga jengo la kiwanda, kuingiza umeme, maji na ununuzi wa tenki la kupoza maziwa (chilling tank) lenye uwezo wa lita 2,030.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uibuaji wa ujenzi wa Kiwanda cha Maziwa cha Isange ulitokana na ukosefu wa soko la maziwa na hivyo kufanya maziwa mengi kuharibika. Hata hivyo, ujenzi wa kiwanda ulikwama baada ya kumalizika kwa Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Kwanza (ASDP I) ambayo ilikuwa ikifadhili mradi wa kiwanda hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Busokelo ilitangaza fursa ya uwepo wa jengo la Kiwanda cha Maziwa kwa ajili ya wawekezaji ambapo mwekezaji ASAS DAIRIES LTD alijitokeza na kuomba kuwekeza katika jengo la Kiwanda cha Maziwa. Mwekezaji baada ya kuingia mkataba na halmashauri ameanza kutumia jengo hilo kama Kituo kikubwa cha kukusanyia maziwa yanayonunuliwa kutoka kwa wafugaji kupitia Ushirika wa Wafugaji wa Maziwa wa UTAMBUZI. Kwa sasa mwekezaji anakusanya jumla ya lita 3,600 za maziwa kwa siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji ameahidi kufunga mitambo ya kuchakata maziwa kama kiasi cha maziwa kitaendelea kuongezeka. Hivyo, naomba kutoa wito kwa wafugaji wa huko Busekelo kutumia fursa hii kuongeza uzalishaji wa maziwa.
MHE. SUSANNE P. MASELLE aliuliza:-
Mnamo tarehe 30 Januari, 2017, wavuvi wa maeneo ya Igombe na Ilemela Jijini Mwanza walikamatwa na kunyang’anywa nyavu, mitumbwi na mashine za mitumbwi yao na Maafisa wa Uvuvi wakidai wanatumia nyavu haramu ambazo ni “double” huku Serikali ikitaka watumie “single”:-
(i) Je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kutoa taarifa, elimu na muda kwa wavuvi pindi inapotaka wavuvi wafanye mabadiliko katika shughuli au zana zao za kazi?
(ii) Je, ni lini Serikali itatoa elimu kwa wavuvi wa Igombe na maeneo mengine ya Mwanza kuhusiana na uvuvi wa kutumia nyavu za single badala ya double ili wafanye kazi zao kwa uhuru bila bughudha ya kukamatwakamatwa?
(iii) Je, Serikali inataka wavuvi wavue samaki katika kina kipi cha maji na katika kina cha mita 50 na kuendelea watumie nyavu za mita ngapi kwenda chini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susane Peter Maselle, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutoa taarifa na elimu kwa wavuvi kuhusiana na usimamizi endelevu wa rasilimali za uvuvi kupitia mikutano, vipindi vya redio na runinga. Pia, leseni za uvuvi huonyesha masharti yanayopaswa kufuatwa ili kuwa na uvuvi endelevu. Kimsingi elimu kwa wavuvi hutolewa kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na wakati wanapopewa leseni na wakati wa kutoa huduma za ugani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kutumia Maafisa Uvuvi wa Idara, Manispaa ya Ilemela na Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU) imeendelea kutoa elimu kwa wavuvi wa Igombe na maeneo ya Mwanza juu ya katazo la matumizi ya nyavu za kuunga kwa maana ya double.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wanaweza kuvua katika tabaka lolote la maji kwa kutumia nyavu zinazoruhusiwa. Isipokuwa hawaruhusiwi kuvua katika maeneo ya mazalia ya samaki na maeneo tengefu. Aidha, katika kina cha mita 50, wavuvi wanapaswa kutumia nyavu zilizoruhusiwa zisizozidi macho au matundu 26 kwenda chini kwa upande wa Ziwa Victoria.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Eneo la tambarare la Tarafa ya Umba na Mkomazi hususan Vijiji vya Mkundi - Mbaru, Mkundi - Mtae lina miundombinu ya majosho ya mifugo na malambo ya kunyweshea mifugo iliyo chakavu.
a) Je, ni lini sasa Serikali itaboresha miundombinu hii ili ipunguze adha ya wafugaji kuhangaika?
b) Kwa kuwa eneo hili ni la wafugaji tangu mwaka 1954, je, ni lini sasa Serikali italiwekea mpaka rasmi ili kupunguza migogoro isiyokwisha ya wafugaji na wakulima?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza uniruhusu nikutakie heri ya siku yako ya kuzaliwa hii leo na baada ya kukutakia heri ya siku yako ya kuzaliwa, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa 2016/2017 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ilijenga birika la maji la kunywea mifugo katika Kijiji cha Kamba kupitia miradi ya maji ya kunywa vijijini. Pia mwaka 2017/2018 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kwa kushirikiana na wafugaji ilikarabati josho na birika la kunywea mifugo katika Kijiji cha Kivingo kwa gharama ya shilingi milioni 12.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 kiasi cha shilingi milioni 4.8 zilimetengwa kwa ajili ya kukarabati majosho mawili katika Vijiji vya Mkundi-Mtae na Kiwanja ili kupunguza adha ya wafugaji kuhangaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto imetenga shilingi milioni kumi kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi katika Vijiji vya Mkundi - Mtae, Mkundi - Mbaru na Kivingo. Aidha, utekelezaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi utahusisha uwekaji wa alama za kudumu kwa maana (beacon) pamoja na uendelezaji wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho kwa kuweka miundombinu muhimu ya mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito kwa Halmashauri zote nchini kuweka mipango ya matumizi bora ya ardhi ili kupunguza migogoro kati ya wafugaji, wakulima na watumiaji wengine wa ardhi.
MHE. KABWE R. Z. ZITTO aliuliza:-

(a) Je, ni kwa nini Serikali ya Tanzania inazuia wawekezaji wa uvuvi kuvua kwa kutumia purseiner katika Ziwa Tanganyika ilhali nchi za Burundi, Zambia na DRC zinazopakana na ziwa hilo huruhusu uvuvi huo?

(b) Je, kwa nini Serikali inawaelekeza wawekezaji wa uvuvi katika Ziwa Tanganyika kuhamisha uwekezaji wao na kuupeleka mahali pengine nchini na je, huu sio makakati wa kukwamisha maendeleo ya Mkoa wa Kigoma na watu wake?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Zitto Ruyagwa Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini lenye kipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimwa Naibu Spika, si lengo la Serikali kuzuia uwekezaji wa uvuvi wa kutumia purseiner katika Ziwa Tanganyika. Serikali katika kuhakikisha kuwa wananchi wake husuani wavuvi wadogo na wazawa wananufaika na rasimali za uvuvi katika kuwaletea maendeleo, inazingatia msingi ya uvunaji endelevu unaoendana na wingi wa rasilimali zilizopo.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, tathimini ya wingi wa rasimali za uvuvi katika Ziwa Tanganyika (stock assessment) iliyofanya mwaka 1998 ilionesha wingi wa samaki ulikadiriwa kuwa tani 295,000. Serikali inaendelea kufanya tafiti mbalimbali ili kuweza kujua wingi wa samaki kwa sasa kabla ya kuridhia shughuli za uvuvi mkubwa ili usiathiri wavuvi wadogo wadogo, wananchi wa kawaida na mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, si kweli kuwa Serikali ina mkakata wa kukwamisha maendeleo ya Mkoa wa Kigoma na watu wake, isipokuwa kwa sasa hatuna hakika na wingi wa samaki uliopo katika Ziwa Tanganyika kwani mara ya mwisho tafiti ya tathimini ya wingi wa samaki ilifanyika ya Ziwa Tanganyika ilifanyika mwaka 1998. Iwapo tafiti itaridhia uvuvi huu bila kufanya tathmini ya wingi wa samaki wadogo, wazawa wa Kigoma na mazingira yanawaweza yakaathirika.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-

Serikali ilikuwa na nia kuanzisha Ranchi za Taifa katika maeneo mbalimbali.

(a) Je, kuna ranchi ngapi na kati ya hizo ngapi zimebinafsishwa na ngapi zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa?

(b) Kwa siku za nyuma Ranchi ya Kongwa na Ranchi ya Ruvu, mifugo ilikuwa inaonekana hata ukipita barabarani hali hiyo sasa haipo, je, kuna tatizo gani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya Ranchi za Taifa ilianzishwa mwaka 1968 kwa Sheria ya Makampuni (Cap 212) kwa lengo la kuendeleza ufugaji wa mifugo bora ya nyama ili kitosheleze mahitaji ya nyama ndani na ziada ya kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, NARCO inamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 ikiwa chini ya usimamizi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Aidha, NARCO inamilikiwa jumla ya ranchi 14 zenye ukubwa wa hekta 544,207 zilizotawanyika sehemu mbalimbali nchini ambazo zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa siku za nyuma Ranchi za Ruvu na Kongwa zilikuwa na idadi kubwa ya mifugo ambayo ilionekana hata ukiwa barabarani. Hata hivyo, Kampuni ya Ranchi za Taifa impitia changamoto mbalimbali ikiwemo mwaka 1992 kupendekezwa kubinafsishwa na kuwa nchini ya uangalizi wa Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashiriki ya Umaa (PSRC) kwa miaka 14. Katika kipindi hicho kampuni haikutekeleza shughuli za maendeleo na hivyo kupelekea uchakavu wa miundombinu na mashamba kuvamiwa, vichaka na mifugo kupungua. Aidha, kampuni inafanya jitihada za kuboresha miundombinu na malisho katika ranchi hizi ili kuirejesha hali ya kuwa na mifugo mingi.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI aliuliza:-

Uvuvi haramu bado unaendelea licha ya adhabu kubwa inayotolewa kwa watu wamaojihusisha nao.

(a) Je, Serikali ina mkakati gani katika kuwasaidia wananchi wake fursa zilizopo badala ya kutoa adhabu kali zinazowaumiza?

(b) Je, Serikali inavisaidiaje vikundi vya Beach Mananagement Unit vinavyojihusisha kuona faida ya kazi wazofanya?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mikakati mbalimbali ya kuwasaidia wananchi wake wanaojihusisha na uvuvi ikiwemo:-

(i) Kufata kodi mbalimbali ili kuwapunguzia wavuvi mzigo kama vile Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye injili za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu, nyavu za uvuvi na vifungashio kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2011 na Sheria ya Mamlaka ya Mapato (VAT Act) ya mwaka 2014.

(ii) Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile tunao mkakati wa kupunguza au kuondoa ushuru na tozo mbalimbali kama vile ushuru wa usajili kwa vyombo vya uvuvi vilivyo chini ya mita 11 na tozo ya cheti na afya nazo zimeondolea.

(iii) Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati mwingine ni kuhakikisha wavuvi wanaanzisha vyama vya ushirika ili waweza kunufaika na programu mbalimbali, mfano wavuvi scheme iliyopo katika Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa (NSSF).

(iv) Kufanya maboresho ya sheria na kanuni za uvuvi ili ziweze kuendena na mazingira na hali ya sasa ya uvuvi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia inafanya yafuatayo ili kuvisaidi vikundi vya vya uvuvi shirikishi wa mazingira ya bahari na maziwa yaani BMUs.

(i) Kuvipatia elemu na kuvijenge uwezo wa kusimamia rasilimali za uvuvi kwa lengo la kuwa na uvuvi endelevu.

(ii) Kuziagiza Halmashauri za Wilaya zote nchini kuvipatia vikundi vya BMUs uwakala wa kukusanya mapato yatokanayo na uvuvi katika Halmashauri zao.
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-

Katika Jimbo la Kibiti kuna mifugo mingi kama ng’ombe, mbuzi na kondoo, hivyo kusababisha mtafaruku baina ya wakulima na wafugaji, kwani wafugaji hawajawekewa mazingira rafiki kwa mifugo yao:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha mazingira rafiki kwa mfugaji?

(b) Je, ni lini mazingira hayo yataboreshwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kibiti ni moja ya Wilaya nane zilizopo katika Mkoa wa Pwani. Wilaya hii ina mifugo takribani Ng’ombe 50,000, Mbuzi 8,852 na Kondoo 4,877. Serikali inao mkakati wa kuboresha mazingira rafiki kwa wafugaji wa Wilaya ya Kibiti kwa kufanya mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 80 kwa ajili ya kuanzisha minada miwili ya awali ambapo wafugaji watapata mahali pa kuuzia mifugo yao, Shilingi milioni 18 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa machinjio; na jumla ya shilingi milioni sita zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa josho. Aidha, Wilaya ya Kibiti kupitia Serikali za Vijiji imetenga takribani hecta 22,000 kwa ajili ya wafugaji katika vijiji18.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yaliyotengwa yatawezesha wafugaji kupata malisho na machunga. Wataalam wameendelea kuwahamasisha wafugaji kushiriki katika kuboresha maeneo yaliyotengwa na kusisitiza wakulima wasivamie maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafugaji. Pia, mifugo ifugwe kulingana na ukubwa wa eneo na pale inapozidi, basi ivunwe ili kuendana na hali halisi ya ukubwa wa eneo.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeandaa mikakati ya kuendeleza sekta ya mifugo nchini katika Wilaya ya Kibiti ikihusisha uboreshaji wa malisho, ujenzi wa majosho, minada ya awali, machinjio na miundombinu ya maji kwa mifugo na utekelezaji wake, unatarajiwa kuanza hivi karibuni kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. DAIMU I. MPAKATE (K.n.y. MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO) aliuliza:-

Idadi ya watu nchini inazidi kuongezeka sambamba na ongezeko la mahitaji ya ardhi kwa ajili ya kilimo na ufugaji:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea uwezo wakulima na wafugaji ili kuendeleza shughuli zao kwa tija na kuwaondolea adha wanazozipata?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sikudhani Yassin Chikambo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu ufugaji bora na uzalishaji wa malisho kupitia mashamba darasa ili kuwajengea uwezo wa kufuga kwa tija pamoja na kuendeleza malisho katika maeneo yaliyotengwa. Lengo la kutoa elimu hii ni kuhakikisha wafugaji wanaachana na ufugaji wa kuhamahama na kutulia kwenye eneo moja lenye malisho yaliyoboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya mashamba darasa 265 yameanzishwa katika Halmashauri mbalimbali nchini ambapo wafugaji wanaweza kujifunza jinsi ya kuzalisha mbegu na malisho bora ya mifugo ili kuongeza upatikanaji wa uhakika wa mbegu na malisho ya mifugo. Aidha, katika mwaka wa 2018/2019, Serikali imeongeza hekta 2,500 katika mashamba yake kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu za malisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imepanga kutoa mafunzo rejea kwa wafugaji na Maafisa Ugani nchi nzima juu ya ufugaji bora unaozingatia ukubwa wa ardhi iliyopo. Mafunzo hayo tayari yameanza kutolewa katika Halmashauri ya Simanjiro, Mkoani Manyara na Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua, Mkoani Tabora na kuendelea kutolewa kwa awamu katika Halmashauri zote nchini. Aidha, Serikali imeendelea na juhudi za kuwasaidia wafugaji kukabiliana na tatizo la maji kwa ajili ya mifugo kwa kuchimba malambo 1,381 na visima virefu 103 katika Halmashauri mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Mawaziri nane iliyoundwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kutafuta suluhu ya migogoro ya matumizi ya ardhi iliyoko nchini tunaamini itakuja na mapendekezo chanya ambayo yatapelekea kuondoa migogoro na adha zinazowakabili wafugaji na wakulima nchini.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-

Kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na.22 ya mwaka 2003, Dagaa wanapaswa kuvuliwa kwa wavu wenye matundu mm 8 – mm10, lakini sheria hii haijazingatia aina tofauti za dagaa:-

Je, kwa nini Serikali isifanye utafiti utakaoainisha matumizi ya nyavu kutegemea aina ya dagaa wanaopatikana kwenye Ziwa husika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi ina jukumu la kulinda, kuhifadhi na kuendeleza na kuhakikisha kuwa rasilimali za uvuvi hapa nchini zinavunwa kwa busara ili ziwe endelevu kwa manufaa ya kiuchumi, kijamii na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria na kanuni zinazosimamia uvuvi nchini zinalenga uvuvi unaofanyika uwe endelevu ambapo Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) hufanya tafiti ili kubaini athari za matumizi ya dhana na mbinu mbalimbali za uvuvi kwa rasilimali za uvuvi na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 66(1)(k) cha Kanuni za Uvuvi za mwaka 2009 kinaeleza kuwa nyavu za dagaa zenye ukubwa wa machi chini ya milimita nane zimakatazwa kutumika kwa uvuvi wa dagaa katika maji baridi ikiwemo Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa. Aidha, tafiti zilizofanyika katika Ziwa victoria zinaonesha kuwa aina moja tu ya dagaa anayejulikana kwa jina la kitaalam Rastrineobola argentea. Utafiti pia unaonesha nyavu zenye macho kuanzia milimita nane zikitumika kuvua dagaa hawa Ziwa Victoria zitavua dagaa waliopevuka na matumizi ya nyavu zenye matundu chini ya milimita nane zikitumika zitavua dagaa wachanga na hii itaathiri uvuvi wa dagaa katika Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Uvuvi na Kanuni zake imezingatia aina ya dagaa katika maji baridi na maji bahari. Aidha, TAFIRI itafanya utafiti ikiridhika kuna haja ya kufanya hivyo katika Ziwa Victoria kuhusiana na uvuvi wa dagaa. Serikali inaendelea kusisitiza wavuvi kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.
MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-

Zamani kulikuwa na maeneo yaliyokuwa yametengwa kwa ajili ya Mifugo na Kilimo katika kutekeleza Sera ya Matumizi Bora ya Ardhi, lakini idadi ya watu inavyoongezeka, maeneo hayo yanavamiwa na kusababisha migogoro:-

Je, Serikali ina mpango gani juu ya kuanzisha Skimu ya Ufugaji bora na kilimo cha kisasa ili kuepukana na migogoro ya wakulima na wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alex Raphael Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hapo awali yalikuwepo maeneo mengi yaliyokuwa yametengwa kwa ajili ya wafugaji nchini ambayo kwa sasa yamepungua kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ongezeko la shughuli za kijamii kama vile kilimo, makazi na shughuli nyingine za kiuchumi. Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri mbalimbali nchini imetenga maeneo ya malisho kuyagawa kwenye vitalu na kuyatoa kwa wafugaji kwa ajili ya malisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jukumu la kuanzisha “Scheme” za ufugaji wa kisasa unaozingatia kanuni za ufugaji wa kisasa, Serikali kupitia Wakala wa Mafunzo ya Mifugo Nchini (LITA) imeandaa mpango kabambe wa kuanzisha “Incubation Youth Center “ambapo vijana waliohitimu Vyuo vya katika ngazi ya Cheti na Diploma watapata fursa ya kuanzisha miradi ya ufugaji kwa vitendo kwa muda maalum chini ya wakala na watakapohitimu watakuwa na fursa nzuri ya kujiajiri kupitia ufugaji. Pia, watakuwa na fursa ya kuanzisha mashamba ya mfano katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imezindua rasmi mafunzo rejea kwa Maafisa Ugani na Wafugaji kuhusu ufugaji bora nchini nchi nzima. Mafunzo hayo yanakusudiwa kutolewa kwenye Halmashauri zote nchini na yameanza kutolewa katika Wilaya ya Simanjiro, Mkoani Manyara ambapo wafugaji 750, Maafisa Ugani 32 walipata mafunzo rejea na katika Wilaya ya Kaliua, Mkoa Tabora mafunzo rejea yalitolewa kwa wafugaji 438 na Maafisa Ugani 33.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafunzo hayo yamejikita katika uboreshaji wa Kosaafu za mifugo, udhibiti wa magonjwa, matumizi sahihi ya madawa na viuatilifu, uboreshaji wa viuatifu, uelewa wa Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Mifugo ili kuepukana na migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

Aidha, mafunzo yanalenga kuwaongezea wafugaji maarifa kwa kuwapatia teknolojia mpya ili kuhamasisha Ufugaji wa Kisasa na Wakibiashara nchini. Mpango huu unalenga kuongeza uzalishaji wa malighafi zitokanazo na mifugo yenye viwango bora ili kukidhi mahitaji ya viwanda vya nyama maziwa na ngozi vinavyoendelea kujengwa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na juhudi hizo, Wizara imeendelea kuhamasisha wafugaji kuanzisha maeneo ya kuzalisha malisho bora ili kuongeza uzalishaji. Pia Wizara imeanzisha mashamba darasa ya mfano 365 katika maeneo mbalimbali nchini ili kuchochea wafugaji kujifunza na kuzalisha mbegu na malisho.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM aliuliza:-

Uvuvi ni moja ya vipaumbele vinavyosaidia kusukuma maendeleo ya wananchi wengi wa Tanzania na Taifa letu ni miongoni mwa Mataifa maskini duniani:-

Je, Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga namna gani katika kuwasaidia wavuvi wadogo ili kukuza maendeleo ya Taifa pamoja na kujikwamua na umasikini uliokithiri?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Salim Maalim, Mbunge wa Kojani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ina mikakati mbalimbali inayolenga kuleta maendeleo katika Sekta ya Uvuvi na kuwasaidia wavuvi ambayo ni pamoja na:-


(i) Kufanya mapitio ya Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 ili kuendana na Sera ya Uvuvi ya mwaka 2015 na mabadiliko ya sasa ili kulinda, kusimamia, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za uvuvi nchini kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

(ii) Kuwekeza katika uvuvi wa Bahari Kuu kwa kufufua Shirika la Uvuvi la TAFICO, kujenga bandari ya uvuvi na kununua meli mbili kubwa za uvuvi ili kuchochea ukuaji wa viwanda vya kuchakata samaki, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, ajira na kuongeza mapato ya Serikali;

(iii) Kutoa elimu kwa wavuvi kuhusu uvuvi endelevu, ukuzaji viumbe katika maji na ufugaji samaki kwenye vizimba kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa samaki ndani ya nchi; na

(iv) Kufanya tafiti mbalimbali zitakazosaidia kuendeleza Sekta ya Uvuvi Nchini.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeanzisha Dawati la Sekta Binafsi ili kuwasaidia wavuvi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo kupata mikopo kutoka Taasisi za Fedha. Pia Serikali inaendelea kuwahimiza wavuvi kujiunga katika vikundi na kuanzisha Vyama vya Ushirika vya Msingi, Vyama vya Akiba na Mikopo na VICOBA ili waweze kukopesheka na kuweza kununua zana na vyombo bora vya uvuvi.
MHE. MBARAKA K. DAU Aliuliza:-

Je, ni kiasi gani cha fedha kimepatikana mpaka sasa kwenye tozo (entrance fee) ya kuingia maeneo ya Hifadhi ya Bahari (Marine Park) katika Kisiwa cha Mafia?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu Na. 29 ya mwaka 1994, imekipa Kitengo cha Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu mamlaka ya kukusanyafedha zitokanazo na shughuli za utalii kwenye maeneo yaliyohifadhiwa (Hifazi za Bahari na Maeneo Tengefu) kwa ajili ya uanzishaji, usimamizi na uendelezaji wa maeneo yaliyohifadhiwa.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi kuanzia mwaka 2000 hadi mwaka 2001 mpaka kufika mwaka 2017/2018, Hifadhi ya Bahari ya Mafia imekusanya jumla ya fedha Sh.6,140,843,478 za Kitanzania, zilizotokana na tozo za viingilio kwa wageni walioingia kwenye hifadhi ya bahari ya Mafia kwa kipindi hicho.
MHE. JULIUS K. LAIZER aliuliza:-

Tanzania ni nchi ya tatu (3) Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya takribani mifugo milioni 25 lakini sekta hii bado mchango wake katika pato la Taifa ni ndogo ukilinganisha na idadi ya mifugo tuliyonayo:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga viwanda vya nyama, ngozi na maziwa hapa nchini ili kuongeza thamani ya mazao yatokanayo na mifugo?

(b) Je, ni lini Serikali itaanza kutoa ruzuku ya madawa kama Ndigana Kali, Homa ya Mapafu na dipu kwa wafugaji wetu nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ina mkakati wa kuendeleza Sekta ya Mifugo nchini kwa kuboresha kosaafu, malisho, kuelimisha wafugaji kuhusu ufugaji wa kisasa, kuimarisha utafiti na kuweka mazingira bora ya kuvutia wawekezaji katika ujenzi wa viwanda vya kusindika na kuongeza thamani mazao ya mifugo. Aidha, Wizara kupitia Taasisi ya NARCO imeingia mkataba na Kampuni ya NECAI ya Misri kujenga kiwanda cha kusindika na kuongeza thamani ya mazao ya mifugo katika Mkoa wa Pwani (Ruvu). Aidha, viwanda kumi na nne (14) vya nyama na maziwa vipo katika hatua mbalimbali za ujenzi kikiwemo kiwanda cha kisasa cha Elia Foods Overseas Ltd kinachojengwa katika Wilaya ya Longido kitakachokuwa na uwezo wa kuchinja ng’ombe 400 na mbuzi 2,000 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mkakati wa kudhibiti magonjwa ya mifugo, Wizara imenunua na kusambaza kiasi cha lita 8,823 za dawa ya kuogesha mifugo (dipu) kwa ruzuku ya asilimia 100 katika mikoa yote ya Tanzania Bara. Aidha, Serikali imewezesha uzalishaji wa chanjo muhimu nchini zikiwemo chanjo za Homa ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP) kupitia Taasisi ya TVLA pamoja na kuanzisha mfumo wa ununuzi wa dawa, chanjo na viwatilifu kwa pamoja (Bulk Procurement) ili kurahisisha usimamizi na upatikanaji wa pembejeo hizi kwa urahisi na kwa bei nafuu.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. AUGUSTINE V. HOLLE) aliuliza:-

Migogoro ya wafugaji na wakulima nchini imekuwa ya kudumu na hivyo kusababisha vifo kwa watu na uharibifu wa mali:-

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka kuja na Sera ya kupunguza idadi ya mifugo nchini ili kuwa na ufugaji wenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustine Vuma Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi inatekeleza mpango wa kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu ufugaji bora na uzalishaji wa malisho kupitia mashamba darasa ili kufuga kwa tija pamoja na kuendeleza malisho katika maeneo yaliyotengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu inayotolewa itawezesha uboreshaji wa kosaafu za mifugo, udhibiti wa magonjwa, matumizi sahihi ya madawa na viuatilifu, uelewa wa sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya mifugo ili kuepukana na migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

Aidha, elimu inalenga kuwaongezea wafugaji maarifa kwa kuwapatia teknolojia mpya ili kuhamasisha ufugaji wa kisasa na kibiashara nchini. Pia elimu hiyo itasaidia kuongeza uzalishaji wa malighafi zitokanazo na mifugo zenye viwango bora ili kukidhi mahitaji ya viwanda vya vyama, maziwa na ngozi vinavyoendelea kujengwa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ina mpango wa kufanya mapitio ya sera ya Taifa ya mifugo ya mwaka 2006 ili iweze kuendana na mabadiliko ya mazingira ya sasa.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-

Tanzania imebarikiwa kuwa na Ukanda wa Bahari na Maziwa.

Je, wananchi wa maeneo hayo wameandaliwaje kufaidika na rasilimali zinazopatikana katika Ukanda wa Bahari na Maziwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sekta ya uvuvi nchini inasimiwa na sera, sheria pamoja na miongozo mbalimbali iliyoandaliwa kwa lengo la kuhakikishwa wananchi na Taifa linanufaika na rasilimali za uvuvi. Pia Sera ya Uvuvi inaelekeza ushirikishwaji wa wananchi katika kusimamia rasilimali za uvuvi ambapo vimeanzishwa vikundi vya usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi kwa maana ya BMU. Vikundi hivi vinalenga kuwawezesha wananchi katika maeneo vilipoanzishwa kuwa wanufaikaji wa kwanza wa rasilimali hizi kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali ya uvuvi endelevu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanzisha Wakala wa Mafunzo ya Uvuvi ili kuwapatia elimu vijana wa Kitanzania kuhusu masuala ya uvuvi ili nchi inufaike na rasilimali za uvuvi tulizojaliwa. Pia, Serikali imeanzisha Taasisi ya Utafiti yaani TAFIRI ili kufanya tafiti na kuvumbua teknolojia zitakazosaidia kuleta tija kwenye tasnia ya uvuvi. Taasisi hizi husaidia kuwapatia elimu na maarifa wadau wa uvuvi.

Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara ina mikakati mbalimbali inayolenga kuleta maendeleo katika sekta ya uvuvi na kuwasaidia wavuvi ambayo ni pamoja na:-

(i) Kuendelea kutoa elimu kwa wavuvi na wadau wote kuhusu uvuvi endelevu, sera, sheria na kanuni za uvuvi ili kulinda, kusimamia, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za uvuvi nchini kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo;

(ii) Kuwekeza katika uvuvi wa bahari kuu kwa kufufua Shirika la Uvuvi (TAFICO), kujenga bandari ya uvuvi, kununua meli mbili kubwa za uvuvi ili kuchochea ukuaji wa viwanda vya kuchakata samaki, kuongeza thamani ya mazao, ajira na kuongeza mapato ya Serikali; na

(iii) Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wavuvi kuhusu ukuzaji wa viumbe katika maji yaani aquaculture na ufugaji samaki kwenye vizimba kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa samaki kwenye maziwa na baharini.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeanzisha Dawati la Sekta Binafsi ili kuwasaidia wavuvi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo kupata mikopo kutoka kwenye taasisi za fedha.
MHE. HAMIDU H. BOBALI (K.n.y. MHE. VEDASTO E. NGOMBALE) aliuliza:-

Zoezi la kupeleka mifugo Mikoa ya Kusini limeleta madhara makubwa kwa mazingira na wananchi kwa ujumla kwa sababu ya kukosa maandalizi kabla ya utekelezaji wake:-

(a) e, Serikali iko tayari kujenga Malambo ili kunusuru tatizo la maji kwa mifugo hiyo?

(b) e, Serikali iko tayari kuondoa mifugo ambayo ipo katika maeneo ambayo hayakupangwa kwa ajili ya mifugo kutokana na mipango ya matumizi bora ya ardhi katika Kata ya Mifola, Kandawale na Somanga?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu maswali ya Mhe. Vedasto Edgar Ngombale Mbunge wa Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa ugetuaji wa Madaraka, kumradhi mnamo mwaka 2006 Serikali iliamua kuondoa makazi, shughuli za kilimo na za mifugo katika bonde la Ihefu ambalo lilikuwa linaendelea kukauka hivyo kuathiri upatikanaji wa maji ya kutosha kwa ajili ya uzalishaji wa umeme. Kabla ya kuondoa mifugo katika maeneo hayo, Ofisi ya Makamu wa Rais ilifanya kikao na Wakuu wa Mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara na Ruvuma kuwaomba waainishe maeneo ambayo yanaweza kutumika kupokea mifugo hiyo. Baada ya kikao hicho Wakuu wa Mikoa hiyo walionesha utayari wa kupokea mifugo katika Mikoa yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua iliyofuata ilikuwa ni kuweka mpango wa matumizi bora ya ardhi ya vijiji ambapo katika Mkoa wa Lindi jumla ya vijiji 69 vilitengeneza mpango wa matumizi bora ya ardhi, na jumla ya Hekta 215,343.34 zilitengwa kwa ajili ya malisho. Serikali pia ilijenga josho na kituo cha kupokea mifugo katika kijiji cha Marendego kilichoko Wilaya ya Kilwa ambapo mifugo ilikuwa inapokelewa na kupatiwa huduma za uogeshaji kabla ya kwenda kwenye vijiji vilivyoandaliwa kupokea mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mujibu wa Sera ya Ugatuaji wa Madaraka, wajibu wa kutoa huduma kwa wafugaji kama vile maji (ujenzi wa mabwawa na malambo) pamoja na majosho ni jukumu la halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iko tayari kushirikiana na halmashauri zenye changamoto kubwa ya ukosefu wa vyanzo vya maji kwa ajili ya mifugo kutegemeana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka 2019/2020, Wizara imepanga kukarabati malambo 6 katika Mikoa ya Manyara, Pwani, Simiyu, Arusha, Geita na Tabora na kuchimba visima virefu 50 katika maeneo yenye mifugo mingi na yaliyotenga maeneo ya malisho ikiwemo Mkoa wa Tunduru- Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mujibu wa Sheria ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya Mwaka 2007, vijiji pia vinayo Mamlaka ya kutunga Sheria ndogo ya kusimamia utekelezaji wa mipango waliojipangia. Kwa sababu hiyo basi, vijiji husika vinao uwezo wa kuondoa mifugo katika maeneo ambayo hayakutengwa kwa ajili ya malisho. Hata hivyo, Wizara imeunda timu ya kutatua migogoro kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi. Aidha, Wizara iko tayari kutumia timu hiyo kwenda jimbo la Kilwa Kaskazini ili kushirikiana na halmashauri katika kutatua tatizo hilo.
MHE. PROF. NORMAN A. S. KING (K.n.y. MHE. NEEMA W. MGAYA) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga kiwanda cha maziwa Wilayani Makete?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Njombe una ng‟ombe wa maziwa 19,759 na idadi kubwa ya ng‟ombe hawa wapo katika Wilaya ya Makete ambapo wanakadiriwa kufikia 8,310.

Katika mwaka 2018/2019 uzalishaji wa maziwa kwa Mkoa wa Njombe ulifikia lita 8,846,496 zinazokadiriwa kuwa na thamani ya shilingi 6,596,925,230/= na wastani wa bei ya maziwa ulikuwa kati ya shilingi 670/= hadi 1,000/= kwa lita moja. Mwaka 2018/2019 Wilaya ya Makete ilizalisha maziwa lita 1,241,550 zinazokadiriwa kuwa na thamani ya shilingi 1,241,550,000/= na kuifanya Wilaya hii kuwa ya tatu kwa uzalishaji wa maziwa katika Wilaya za Mkoa wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla Wilaya ya Mekete inazalisha lita 103,462.5 kwa siku moja. Kwa takwimu hizi ni wazi kwamba maziwa ni bidhaa muhimu kwa kuongeza kipato cha wananchi wa Wilaya ya Makete na Mkoa wa Njombe kiujumla .

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Njombe una kiwanda kimoja cha Maziwa cha Njolifa kilichopo Njombe Mjini chenye uwezo wa kusindika maziwa lita 20,000 kwa siku na mwaka 2018/2019 kilisindika lita 1,620,000. Ni wazi kwamba kiwanda hiki kina uwezo mdogo wa kusindika maziwa ukilinganisha na ma ziwa yanayozalishwa na wafugaji kwa Mkoa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kutambua umuhimu wa tasnia ya maziwa kwa wananchi wa Wilaya ya Makete na nchi kwa ujumla, Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuhamasisha wawekezaji katika Wilaya ya Makete na eneo nzima la Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini. Kwa sasa kiwanda cha ASAS kipo katika hatua za mwisho za upanuzi wa kiwanda chake kipya Wilayani Rungwe.

Mheshimiwa Mwen yekiti, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara na Kituo cha Uwekezaji tunaendelea na kampeni ya kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vya maziwa kwa eneo la ukanda huu ili kuweza kutumia maziwa yote yanayozalishwa Mkoani Njombe ikiwemo Wilaya ya Makete. Hivyo, Wizara inaendelea na jitihada za kuhakikisha mwekezaji mahiri anapatikana ili kuhakikisha maziwa yote yanayozalishwa na Mkoa wa Njombe ikiwemo Wilaya ya Makete na maeneo yanayouzunguka Mkoa huu yanapata soko la uhakika kupitia kiwanda au viwanda vitakavyojengwa.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:-

Serikali iliahidi katika Bajeti ya mwaka 2012/2013 kujenga malambo, majosho na kisima kirefu kwa ajili ya Wananchi wafugaji wa Kata ya Ruvu Jimbo la Same Magharibi?

Je, ni lini ahadi hiyo itakamilishwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mhe. Dkt. David Mathayo Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia bajeti yake pamoja na program mbalimbali imeendelea kukarabati na kujenga miundombinu ya maji ya mifugo katika maeneo mengi ya ufugaji hapa nchini ili kupunguza tatizo la maji hasa wakati wa kiangazi kikali. Katika Mwaka huu wa Fedha 2019/2020 Wizara imetenga fedha Jumla ya shilingi 700,000,000 kwa ajili ya kujenga visima kumi na kukarabati mabwawa kumi katika mikoa kumi Tanzania Bara. Katika utekelezaji wa mpango huo, kisima kimoja kinatarajiwa kuchimbwa katika Wilaya ya Same, hususan Kata ya Ruvu ili wafugaji waweze kupata maji kwa ajili ya mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha 2019/2020 Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kukarabati majosho 161 nchi nzima ili kudhibiti magonjwa yaenezwayo na kupe, mbung‟o na wadudu wengine. Mpaka sasa, majosho 46 yamekamilika, majosho 95 ukarabati unaendelea na majosho 20 ukarabati bado haujaanza. Aidha Wizara imejenga josho moja la kisasa Wilayani Bariadi. Pia Halmashauri mbalimbali zinakarabati majosho 288 na zinajenga majosho mapya 84. Kwa Halmashauri ya Same josho moja linakarabatiwa na Wizara katika Kata ya Ruvu-Muungano na matatu yanakaribatiwa na Halmashauri yaliyopo kwenye vijiji vya Mwembe, Bangalala na Mkonga. Mikakati ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya mifugo inaendelea kadri fedha zinapopatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Napenda kuchukua fursa hii kutoa rai kwa halmashauri zote hapa nchini ikiwemo Halmashauri ya Same kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya kujenga, kukarabati na kuendeleza miundombinu ya mifugo katika maeneo yao kwa kutumia fedha zinazopatikana kutokana na makusanyo ama tozo za mifugo.
MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-

Ranchi za Taifa ni rasilimali muhimu na fursa kubwa katika kuchangia Pato la Taifa na Uchumi wa nchi yetu:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza thamani ya mazao ya mifugo iliyopo kwenye ranchi zetu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kampuni ya ranchi za Taifa (NARCO) imeandaa Mpango Mkakati wa Kibiashara wa miaka mitano kuanzia mwaka 2017/2018 – 2021 – 2022 kwa lengo la kuendeleza na kueneza ufugaji bora hususan ufugaji wa ng’ombe bora wa nyama (boran) kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi kwa kutumia mbinu za kisasa. Maeneo ya kipaumbele katika mpango mkakati huo ni pamoja na kuiwezesha NARCO kuingia ubia na makampuni mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, NARCO imeingia ubia na kampuni ya NICAI ya Misri kwa ajili ya kujenga machinjio ya kisasa na kiwanda cha kuchakata mazao mbalimbali ya mifugo. Aidha, NARCO imeomba fedha kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa la Kilimo na Chakula (IFAD) kiasi cha shilingi bilioni 20 ambapo andiko la mradi (concept note) kwa ajili ya kuendeleza ranchi nane za NARCO limepitishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuongeza idadi ya mifugo ikiwemo ng’ombe wazazi kufikia 20,000 katika kipindi cha miaka mitano ili kuwa na uzalishaji endelevu wa kibiashara. Kuanzisha utaratibu wa kukodisha vitalu ambapo wafugaji wanaomilikishwa vitalu lazima kupatiwa mafunzo ya ufugaji wa kisasa ikiwemo unenepeshaji wa mifugo ili kuongeza uhakika wa upatikanaji wa malighafi za viwandani kama vile nyama, maziwa na ngozi. Ranchi za NARCO zote zitajenga madarasa maalum kwa ajili ya mafunzo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na juhusi za kufanya maboresho makubwa ya NARCO ili kuongeza uwezo wa mtaji, ufanisi na tija hasa kufikia lengo la kuchakata mazao ya mifugo yetu nchini na kufikia masoko ya ndani na ya kikanda.
MHE. JUMA ALI JUMA aliuliza:-

Serikali imezuia kutoa leseni kwa sababu ya ubadhirifu uliokuwa ukifanywa na taasisi za utoaji leseni, hivyo kusababisha kupoteza mapato mengi ya Serikali na kuifanya Taasisi ya Uvuvi wa Bahari Kuu kushindwa kufanya kazi zake inavyotakiwa:-

(a) Je, ni lini Serikali itamaliza mchakato wa kujipanga na kuanza kutoa leseni?

(b) Je, Taasisi ya Uvuvi wa Bahari Kuu imesaidiwa kwa kiasi gani ili iweze kujiendesha kwa kipindi hicho ambacho haikupata mgao utokanao na leseni?
NAIBU WAZIRI WA M IFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Ali Juma, Mbunge wa Dimani, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilisimamisha utoaji wa leseni za uvuvi wa Bahari Kuu kuanzia tarehe 8 Agosti, 2016 mpaka Desemba, 2016 ili kuruhusu marekebisho ya Kanuni za Uvuvi wa Bahari Kuu za mwaka 2009 yakiwemo maboresho ya masharti ya leseni yaliyopo katika kifungu cha 10 ya kanuni za mwaka 2009 na kanuni za kusimamia uvuvi wa Bahari Kuu kwa lengo la kuongeza mapato ya Serikali. Kufuatia marekebisho hayo, wamiliki wa meli zinazovua katika Bahari Kuu wamesita kukata leseni kutokana na kutokukubaliana na masharti mapya yaliyoongezwa katika Kanuni mpya za mwaka 2016.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na Sheria ya Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu ya Mwaka 1998 na Marekebisho yake ya mwaka 2007, mamlaka hupatiwa asilimia 50 ya mapato yote yanayokusanywa kwa mwaka. Ni kutokana na bakaa (akiba) ya mgao huo mamlaka imeendelea kujiendesha na kutimiza wajibu wake kwa mujibu wa sheria. Aidha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zipo kwenye hatua za mwisho kutatua changamoto ya meli za uvuvi kutokukata leseni na kuiwezesha mamlaka hii kujiendesha.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:-

Je, ni hatua zipi zimechukuliwa hadi sasa kumaliza mgogoro wa mipaka kati ya Ranchi ya Missenyi na Vijiji vinavyopakana na Ranchi?
NAIBU WA WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kamala, Mwalimu wangu kama Ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ranchi ya Missenyi ina eneo lenye hekta 60,851 na lina hati iliyopatikana tarehe mwaka 1969. Ranchi ya Missenyi imepakana na Vijiji vya Kakunyu, Bugango, Bubale na Byeju. Katika kubiliana na mgogoro kati ya vijiji na Ranchi, vijiji hivi vilipewa maeneo kutoka NARCO kama ifuatavyo; kijiji cha Kakunyu kilipewa heka 7,192, Bugango kilipewa heka, 5,849, Bubale heka 3,817, Byeju heka 3,904 kwa ujumla vijiji hivi vinne vilipewa jumla ya heka 20,771.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimeongezwa hekta 800.0 kutoka kitalu Na. 17 na Kitalu Na. 19 na kufanya Jumla ya hekta 21, 571 zilizotolewa kwa vijiji Serikali inapanga kupima upya eneo la Ranchi ya Missenyi kwa lengo la kumaliza mgogoro wa ardhi kati ya Ranchi na vijiji inavyopakana navyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa rai kwa wananchi wa vijiji vinavyopakana na Ranchi ya Missenyi kutoa ushirikiano wa kutosha pindi zoezi la upimaji litakapoanza.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-

Je, ni vikundi au wavuvi wangapi katika Kisiwa cha Ukerewe wamepewa elimu na mitaji ili waweze kufanya uvuvi wenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitoa elimu kwa wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe juu ya uvuvi endelevu, matumizi ya zana na mbinu bora za uvuvi zinazokubalika kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na madhara yatokanayo na uvuvi haramu. Lengo la elimu hiyo ni kuwawezesha wavuvi wadogo wa kisiwa cha Ukerewe kufanya uvuvi endelevu na hivyo kunufaika na rasilimali za uvuvi zilizopo katika maeneo yao. Zaidi ya wavuvi wadogo na wadau wengine wa uvuvi wapatao 520 kutoka visiwa vya Ghana, Kunene, Lyegoba na Hamukoko katika Halmashauri ya Kisiwa cha Ukerewe walipatiwa elimu hiyo kwa njia ya mikutano.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) ili kuwezesha wavuvi kupata mikopo yenye riba nafuu kwa ajili ya kununua zana bora za uvuvi wakiwemo wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe. Ili kuwezesha wavuvi kunufaika na fursa hiyo, Serikali imeendelea kuwahamasisha wavuvi wadogo nchini wakiwemo wa Kisiwa cha Ukerewe, kuunda na kujiunga katika Vikundi vya Ushirika vya Wavuvi na Vyama vya Akiba na Mikopo ili kuwasaidia wavuvi kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha.

Aidha, hadi sasa jumla ya shilingi million 250 zipo katika hatua ya mwisho ya kutolewa kwa wavuvi wa Kisiwa cha Ukerewe kama mkopo kupitia Chama cha Ushirika cha Bugasiga kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, uhamasishaji huo umewezesha kuanzishwa kwa Chama cha Ushirika cha Wavuvi katika Kisiwa cha Ukerewe, visiwa vidogo vya Ghana, Kunene, Lyegoba na Hamukoko ambacho kipo katika hatua za usajili. Uanzishwaji wa chama hiki utawezesha wavuvi kutoka Kisiwa cha Ukerewe kupata mikopo kwa urahisi kutoka Taasisi za Kifedha na hivyo kufanya uvuvi wenye tija.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM (K.n.y. MHE. HAMADI SALIM MAALIM) aliuliza:-

Uvuvi si suala la Muungano na wavuvi wengi wa Visiwa vya Unguja na Pemba wanapokuwa katika maeneo mbalimbali ya mwambao wa Afrika Mashariki hukumbana na changamoto nyingi ikiwemo kukamatwa wanapokuwa katika shughuli zao za uvuvi, kutozwa tozo zisizo za lazima na kadhalika:-

Je, Serikali imejipangia mikakati gani ili kupunguza changamoto hizo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamadi Salim Maalim, Mbunge wa Kojani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa uvuvi katika maji ya ndani na maji ya kitaifa sio suala la Muungano kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo kila upande wa Muungano una sheria, kanuni na miongozo inayosimamia masuala ya uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2018 na 2019 zinaelekeza mvuvi anapohamisha shughuli zake za uvuvi kutoka eneo moja kwenda eneo lingine anapaswa kuwa na leseni na vibali vya kujishughulisha na shughuli za uvuvi na kujitambulisha kwa mamlaka za eneo husika. Vilevile, tozo mbalimbali zinatozwa kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Miongozo iliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imeweka mikakati ya kupunguza na kuondoa kabisa changamoto wanazokumbana nazo wavuvi katika maeneo mbalimbali ya mwambao wa Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuendelea kuwaelimisha wavuvi kuzingatia sheria, kanuni za uvuvi na miongozo iliyopo pamoja na kuheshimu mipaka ya nchi kwa kutovua katika maji ya nchi jirani bila kufuata taratibu zilizowekwa. Aidha, katika kuboresha shughuli za uvuvi na mazao yake, Serikali ipo katika hatua ya kufanyia marekebisho sheria na kanuni za uvuvi ili ziweze kuendana na wakati katika kutunza na kuendeleza rasilimali za uvuvi ili sekta hii iweze kuchangia ipasavyo kwenye Pato la Taifa na la mtu mmoja mmoja.

Vilevile, Serikali imekuwa ikifanya vikao vya ujirani mwema na nchi jirani ili kutatua changamoto zinazojitokeza. Serikali kupitia Mheshimiwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dkt. Ally Mohamed Shein alitukutanisha na viongozi wa Mamlaka za Pwani ya Kenya siku ya tarehe 26 hadi 28 Jijini Nairobi wakati wa Mkutano Mkubwa wa Blue Economy.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza:-

Je, kwa nini uvuvi wa kuzamia kwa kutumia chupa umezuiliwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan King, Mbunge wa Jang’ombe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, shughuli za uvuvi nchini zinasimamiwa kwa mujibu wa Sheria Na.22 ya Mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 na Miongozo mbalimbali ambayo hutolewa kwa ajili ya kusimamia na kuhakikisha kuna matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi. Kwa mujibu wa Kanuni ya Uvuvi ya Mwaka 2009, kifungu cha 66(I – Q), vifaa vya kupumulia chini ya maji au scuba au mitungi ya gesi haviruhusiwi kutumika kwa ajili ya kuvua samaki au viumbe wengine wa baharini. Aidha, kwa mujibu wa kifungu cha 66(2), vifaa vya kupumulia chini ya maji au mitungi ya gesi vinaweza kutumika tu kwa ajili ya uvuvi wa burudani (sport fishing), uvuvi wa samaki wa mapambo, mafunzo na utafiti na ni kwa kibali maalum.

Mheshimiwa Spika, wavuvi haramu wanaotumia milipuko hutumia mitungi ya gesi kuzamia kwa ajili ya kukusanyia samaki waliowaua kutokana na milipuko hiyo. Athari za milipuko ni pamoja na kuharibu matumbawe, (coral reefs) na mazingira ya baharini kwenye maji ambayo ni mazalia na makulia ya samaki pamoja na viumbe wengine na hivyo kuharibu mfumo wa ikolojia ambao unatishia kutoweka kwa kizazi cha samaki. Kuua samaki bila ya kuchagua wakiwemo samaki wachanga na mayai yake na hivyo kuhatarisha uendelevu wa rasilimali za uvuvi nchini.

Pia milipuko husababisha wavuvi kupata ulemavu na hata kifo, hivyo kutokana na sababu hizi Serikali iliamua kupiga marufuku uvuvi wa kutumia chupa au mitungi ya gesi.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA (K.n.y. MHE. PROSPER J. MBENA) aliuliza:-

Kumekuwepo na ongezeko la matukio ya ukatili mkubwa kwa wanyama katika nchi yetu hususan kuku, mbuzi na ng’ombe wakati wakisafirishwa kutoka eneo moja kwenda eneo lingine?

(a) Je, Chama cha kuzuia ukatili wa Wanyama nchini yaani Tanzania Society for the Prevention of Cluelty to Animals (TSPCA) kinashirikiana kwa kiasi gani na Serikali katika kudhibiti vitendo hivyo vya kikatili wa Wanyama?

(b) Je, kwa mwaka 2018 na 2019 ni kesi ngapi zinazohusu matukio ya ukatili kwa Wanyama zilifikishwa Mahakamani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena Mbunge wa Morogoro Kusini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inashirikiana na Mashirika yasiyo ya Kiserikali kama vile TSPCA katika kudhibiti vitendo vya kikatili kwa Wanyama kwa kuzingatia Sera ya Mifugo ya mwaka 2006 na Sheria ya Ustawi wa Wanyama ya mwaka 2008 kwa kuelimisha jamii kuhusu masuala ya Ustawi wa Wanyama. Pia elimu inayotolewa inalenga kuelimisha jamii kuhusu njia sahihi ya usafirishaji mifugo, matumizi ya Wanyama kazi kama punda na kuzuia ukatili wa Wanyama kwenye minada ya mifugo. Aidha, jumla ya wataalam wa mifugo 25 kwenye minada wamepata mafunzo na pia wafanyabiashara wa mifugo takribani 300. Pia, elimu hutolewa kwa njia ya mabango na vipeperushi kwenye minada mikubwa.

Mheshimiwa Spika, Kwa kuzingatia Kifungu namba 60, wanaokiuka Sheria hiyo wanatozwa faini ya papo kwa papo badala ya kupelekwa Mahakamani. Faini hiyo ni shilingi 50,000 kwa kila anayekiuka Sheria hiyo. Kwa mwaka 2018 jumla ya makosa 3,542 kwa kosa la ukatili wa Wanyama yameripotiwa ambayo yamegawanyika kama ifuatavyo; ng’ombe 847, mbuzi na kondoo 1,578, Nguruwe 85, kuku 539 na punda 490.
MHE. TUNZA I. MALAPO (K.n.y. MHE. SAED A. KUBENEA) aliuliza:-

Uvuvi katika nchi yetu ni shughuli inayohusu wakazi wengi sana ikiwa ni ya pili kutoka kwenye kilimo kwa kutoa ajira kwa Watanzania wengi:-

(a) Je, ni lini na ni wapi kiwanda cha samaki kwa ukanda wa Pwani kitajengwa?

(b) Je, mpango wa ujenzi wa Bandari ya Samaki umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea na kuhamasisha Sekta Binafsi kuwekeza katika Sekta ya Uvuvi kwa kuweka mazingira mazuri ikiwemo uwepo wa malighafi kwa viwanda vya kusindika mazao ya uvuvi. Hadi sasa kuna viwanda vitano vya kusindika mazao ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani. Vilevile, Serikali inatarajia kupitia Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) kujenga viwanda vya kusindika mazao ya uvuvi nchini ikiwa ni moja ya mikakati yake.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imeingia mkataba na mshauri elekezi Kampuni ya Sering Ingegneria kutoka Italia kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bandari ya uvuvi katika mwambao wa Pwani ya Bahari ya Hindi. Kampuni hii ilianza kazi tarehe 2 Agosti, 2018 na tayari imekabidhi taarifa ya awali (inception report) na kazi inaendelea ambapo hatua ya pili ya ukusanyaji wa taarifa muhimu (interim report) inaendelea. Aidha, upembuzi huo utakapokamilika utawezesha kutambua maeneo yanayofaa kwa ujenzi wa bandari na gharama za ujenzi wa bandari ya uvuvi.
MHE. SELEMANI S. BUNGARA aliuliza:-

Uvuvi haramu unazidi kushamiri siku hadi siku hasa kwenye maeneo ya Songosongo, Somanga, Njianne, Kivinje hadi Pwani ya Bushungi. Aidha, maeneo haya kuna bomba la gesi linapita na hivyo kujenga hofu ya uwezekano wa mlipuko pamoja na uharibifu wa mazingira kwenye maeneo tajwa.

(a) Je, Serikali ina mpango gani madhubuti kukabiliana na tishio hilo sugu?

(b) Kwa kuwa wanaofanya hujuma hizo wamejiandaa kwa kuwa na boti maalum katika kuendesha huduma hizo; je, Serikali haioni haja ya kuleta boti za doria zenye uwezo wa hali ya juu ili kulinda bahari na bomba la gesi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Said Bungara, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na uvuvi haramu, Wizara inatekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kuanzisha vituo vya doria kwenye maziwa makubwa, mwambao wa Bahari ya Hindi na mipaka ya nchi. Imeanzisha Kikosi Kazi cha Kitaifa (Multi Agency Task Team), ambacho kinafanya kazi ya kudhibiti uhalifu wa mazingira ikiwemo kudhibiti uvuvi haramu hususan matumizi ya mabomu katika shughuli za uvuvi. Kufanya opereshini za mara kwa mara mfano Operesheni Jodari kwenye Ukanda wa Pwani na Operesheni Sangara, Ziwa Victoria, kuanzisha na kuimarisha vikundi vya usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi (BMU) pamoja na kufanya maboresho ya Sheria na Kanuni za Uvuvi ili kuimarisha usimamizi na matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi hapa nchini. Juhudi hizi zimezaa matunda hususan katika Ukanda wa Pwani ambapo uvuvi wa kutumia mabomu kwa maana ya milipuko umepungua kwa takribani asilimia 99.

Mheshimiwa Spika, Serikali itendelea kupambana na tatizo la uvuvi haramu hususan wa mabomu kwa kuhakikisha vituo vya doria vinapatiwa vitendea kazi ikiwemo boti za kisasa ili kuimarisha ulinzi wa rasilimali za uvuvi na miundombinu ya gesi kwa faidi ya kizazi cha sasa na vijavyo.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuiunga mkono Serikali yao kwa kukemea na kupiga vita uvuvi harama katika maeneo yao.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-

Miaka ya karibuni samaki aina ya Ngege (Pelege) katika Ziwa Rukwa wamepungua na kudumaa na hii ni kutokana na uchimbaji wa dhahabu Wilayani Chunya na Songwe ambao mara nyingi ulihusisha zebaki.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kufanya utafiti katika Ziwa hili?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka ya nyuma samaki aina ya ngege katika Ziwa Rukwa walikuwa wanakuwa wakubwa kutokana na kuwa walikuwa hawakabiliwi na changamoto zinazowakabili sasa.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) katika mwaka huu wa 2019 kwenye Ziwa Rukwa, ilibainika kuwa kuna udumavu na upungufu wa samaki katika ziwa hilo na hasa kwa samaki wa jamii ya ngege. ngege aina ya Oreochromis rukwaensis ambaye ni wa asili katika ziwa hilo wamepungua zaidi kulinganisha na ngege aina ya Oreochromis esculentus ambao wamepandikizwa. Udumavu na upungufu wa samaki katika ziwa hilo unasababishwa na changamoto zifuatazo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, uchafuzi wa mazingira utokanao na kuongezeka kwa shughuli za binadamu kama vile:-

(i) Kuongezeka kwa idadi ya mifugo inayotegemea ziwa kupata maji ya kunywa na pia malisho ya mifugo hiyo pembezoni mwa ziwa;

(ii) Kilimo kisichofuata taratibu karibu ama pembezoni mwa ziwa;

(iii) Uchimbaji wa madini ya dhahabu ambapo zebaki, (mercury) hutumika kuchakata dhahabu hizo; na

(iv) Ongezeko la matumizi ya petrol katika machimbo ya dhahabu ambapo petrol hiyo yaweza kusababisha madini ya risasi (lead) kuingia ziwani.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, uvuvi haramu ambao wavuvi hutumia makokoro na nyavu zisizoruhusiwa; Uvuvi haramu usiozingatia taratibu za kulinda rasimali za za uvuvi na mazingira unaendelea kushamiri katika eneo hilo. Uvuvi huo unahusisha makokoro na nyavu zisizoruhusiwa kama vile matumizi ya vyandarua.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sampuli za minofu zimechukuliwa katika Ziwa Rukwa zinaendea kuchakatwa ili kujua kiwango cha zebaki na risasi katika minofu ya samaki na pia kuangalia kiasi hicho kama kipo ndani ya viwango vinavyokubalika na Shirika la Afya Duniani (WHO).
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI aliuliza:-

Tanzania ni kati ya nchi zenye mifugo mingi barani Afrika na sekta hii inaweza kuikwamua nchi kiuchumi:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kurasimisha au kuboresha shughuli za ufugaji nchini ili uwe wa kisasa na wenye tija zaidi badala ya ufugaji wa kuhama hama?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI atajibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mhe shimi wa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, asilimia 97 ya mifugo hufugwa kwa mfumo wa asili ambapo kaya milioni 4.6 sawa na asilimia 50 ya kaya zote vijijini hufuga mifugo. Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kuongeza mchango wa Sekta ya Mifugo kwenye Maendeleo ya Jamii na Pato la Taifa kwa kuleta tija katika uzalishaji, usindikaji na hatimaye soko la mifugo na mazao yake.

Mheshi miwa Spi ka, mikakati inayoendele a kutekelezwa ni pamoja na:-

(i) Mkakati wa kuzalisha wingi ng’ombe bora wa maziwa na nyama kwa njia ya uhimilishaji.

(ii) Mkakati wa upatikanaji wa uhakika wa malisho na maji kwa mifugo.

(iii) Mkakati wa kudhibiti na kuondoa migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

(iv) Mkakati wa udhibiti wa magonjwa ya mifugo kwa njia ya kinga (uogeshaji na chanjo) na tiba.

Mheshimiwa Spika, aidha, Wizara imeendelea kutoa mafunzo juu ya teknolojia sahihi za uzalishaji kwa wafugaji na Maafisa Ugani katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Mifugo ya Wafugaji wakubwa hapa nchini imekosa ubora wa mazao yake kutokana na maradhi ya nayo changi wa na kuko sekana kwa wataalam waliobobea katika fani na kukosa Maabara za Mifugo:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wataalam ama vitendea kazi kama njia mbadala ya kuwasaidia wataalam wachache waliopo kutoa huduma bora kwa wafugaji?

(b) Je, ni lini Serikali itajenga maabara za mifugo katika maeneo ya wafugaji ili wananchi waache kutibu mifugo yao kwa kubahatisha?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin J. Monko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inafanya juhudi za kuongeza idadi ya Maafisa Ugani wa mifugo kwa kuwezesha Wakala wa Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA) kuongeza udahil i wa wanafunzi wa ngazi ya Astashahada na Stashahada katika fani za uzalishaji, afya ya mifugo, nyanda za malisho na maabara kutoka wanafunzi 2,536 mwaka 2018/ 2019 hadi wanafunzi 3,634 mwaka 2019/2020; sawa na ongezeko la wanafunzi 1,098 ambalo ni asilimia 43.3.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mpango wa ujenzi wa maabara za mifugo kwenye kila mkoa. Mpaka sasa kuna maabara za mifugo za Serikali kumi na moja kwenye kila Kanda. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Wizara inategemea kujenga Kliniki za mifugo zenye maabara katika Halmashauri mbili za Chato na Meatu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Wizara imepanga kujenga Kliniki nyingine kumi kwenye Halmashauri mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Sindiga Vijijini.

Mheshimiwa Spika, Wizara pia imeshavielekeza vituo binafsi 1,709 vya kutolea huduma ya afya ya mifugo (Private Veterinary Centers) vilivyopo kwenye Halmashauri zote 185 kuhakikisha vinakuwa na maabara ndogo kwa ajili ya kutoa huduma ya uchunguzi wa awali wa magonjwa ya mifugo.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA Aliuliza: -

Je ni lini Serikali itachukua hatua kudhibiti watu wanaodanganya kupeleka ng’ombe katika mnada wa Mtyangimbole kisha kuwatorosha na kuwaingiza katika maeneo mbalimbali ya Madaba, Namtumbo na Songea ilihali Madaba haina uwezo wa kuhimili wingi wa mifugo hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Madaba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na matumizi mabaya ya vibali vya kusafirisha mifugo kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine ambapo baadhi ya wafugaji wanakata vibali vya kusafirisha mifugo kwenda mnadani kwa ajili ya biashara lakini kinyume chake inahamishwa kuelekea maeneo mengine ya mikoa ukiwemo Mkoa wa Ruvuma, Halmashauri ya Madaba.

Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha kuwa kwa kipindi cha kuanzia Aprili 2020 hadi Aprili 2021 idadi ya idadi ya mifugo iliyosajiliwa katika Halmashauri ya Madaba yenye vibali kuelekea mnada wa upili wa Mtyangimbole ni ng’ombe 8,925 ilhali walioingia mnadani ni ng’ombe 5,753, sawa na tofauti ya ng’ombe 3,172 wanaosadikika kuingia katika maeneo mbalimbali na kusababisha migogoro.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na tazizo hili, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Madaba itaimarisha ufuatiliaji wa vibali vya mifugo ili kuhakikisha mifugo iliyoandikiwa vibali kwenda Mnada wa Mtyangimbole imefika. Vilevile katika kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa malisho na maji kwa mifugo katika maeneo ya wafugaji, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 193.28 kwa ajili ya utatuzi wa migogoro na utengaji wa maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, pia shilingi bilioni 1.586 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa mabwawa/malambo na visima virefu, ambapo katika Mkoa wa Ruvuma, Halmashauri ya Songea, kisima kimoja kitachimbwa kwa lengo la kuwapatia mifugo maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuwahamasisha wadau wengine wakiwemo wafugaji kujiunga kwenye vikundi na kushiriki kwenye ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya maji na uendelezaji wa malisho katika maeneo yaliyotengwa ili kuzuia uhamaji usio wa lazima unaosababisha migogoro.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza: -

Je, ni lini Mnada wa Mifugo wa Magena uliopo Halmashauri ya Mji wa Tarime utafunguliwa kama ambavyo Serikali iliahidi Mwaka 2016?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba uniruhusu, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama katika podium hii, nimshukuru sana Mwenyezi Mungu na pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini kuhudumia katika Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizi, naomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, nijibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mnada wa Mifugo wa Magena, ulikamilika kujengwa mwaka 1995 na kufunguliwa mwaka 1996, ambapo ng’ombe 104,000 waliuzwa na jumla ya Shilingi za Kitanzania 260,000,000/= zilikusanywa kama maduhuli ya Serikali. Hata hivyo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mara mwaka 1997 iliagiza mnada ufungwe kutokana na changamoto zilizojitokeza ikiwemo wizi wa mifugo na sababu za kiusalama. Uongozi wa Mkoa wa Mara uliwasilisha ombi rasmi Wizarani la kufuta mnada wa Magena na kupendekeza mnada huo uhamishiwe eneo la Kirumi Check Point.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ilijenga Mnada wa Kirumi wa Mpakani kwa gharama ya shilingi milioni 321.3 na ulifunguliwa rasmi tarehe 16 Oktoba, 2018. Aidha, tangu uanze kufanya kazi, jumla ya ng’ombe 34,855, mbuzi na kondoo 5,808 wameingia mnadani hapo na jumla ya shilingi milioni 428.9 zimekusanywa kama maduhuli ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia maoni kutoka mamlaka za Mkoa, Wizara itakuwa tayari kuurejesha Mnada wa Magena kwa kufuata taratibu za uanzishwaji upya wa minada na kwa mujibu wa Sheria ya Nyama Na. 10 ya mwaka 2006.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza:-

Je, Serikali ipo tayari kupitia Sera na Sheria ya Uvuvi nchini ambayo inaonekana kutokidhi mahitaji ya wavuvi wadogo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kupitia Sera na Sheria ya Uvuvi nchini na katika kulitekeleza hilo, Wizara imekuwa ikifanya mapitio ya Sera, Sheria na Kanuni za Uvuvi ili ziweze kuendana na mahitaji halisi ya wakati husika na imekuwa ikifanya hivyo mara kwa mara. Kwa mfano, Wizara ilifanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Uvuvi na Mikakati yake ya Mwaka 1997 na kutunga Sera ya Taifa ya Uvuvi ya Mwaka 2015 ambayo imezingatia mahitaji ya wadau wa Sekta ya Uvuvi na Uendelevu wa Rasilimali za Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, aidha, Wizara ilifanya mapitio ya Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania Na. 6 ya Mwaka 1980 na kutunga Sheria Na. 11 ya Mwaka 2016 ili kuimarisha shughuli za utafiti nchini. Pia, katika mwaka 2020 Wizara ilifanya marekebisho madogo kwa maana Miscellaneous amendments kwenye Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 ili kuimarisha shughuli za ulinzi na usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi nchini.

Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kufanya maboresho makubwa kwenye Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 ili iweze kuendana na mahitaji halisi ya sasa ya kisekta ikiwemo kutatua kero mbalimbali za wadau wa Sekta ya Uvuvi hususan wavuvi wadogo na wakuzaji viumbe maji.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kuwa mlipuko wa magonjwa ya nguruwe hayajitokezi mara kwa mara nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika,ni kweli hivi karibuni kulijitokeza mlipuko wa ugonjwa wa homa ya nguruwe katika mikoa kadhaa nchini na kusababisha hasara kwa wafugaji. Ugonjwa huu unaosababishwa na virusi, hauna chanjo wala tiba. Njia pekee za kudhibiti ugonjwa wa homa ya nguruwe ni kuzingatia kanuni bora za ufugaji wa nguruwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali na wadau wengine inafanya jitihada za kudhibiti ugonjwa huu, jitihada hizo ni pamoja na:-

(i) Kuhimiza wafugaji kuacha kufuga nguruwe kwa njia huria;

(ii) Kuzuia wageni kuingia kwenye mabanda ya nguruwe;

(iii) Kuhimiza wafugaji wapulizie dawa za kuua virusi na kupe kwenye mabanda na kuweka dawa ya kuchovya kwenye milango ya mabanda;

(iv) Kuweka katazo la kusafirisha nguruwe na mazao yake kutoka sehemu zenye ugonjwa;

(v) Kuhimiza wafugaji kutokuruhusu wachinjaji au wafanyabiashara kuingia katika mabanda na kuchagua nguruwe wa kununua;

(vi) Kuepuke kulisha nguruwe mabaki ya vyakula kutoka kwenye mahoteli na migahawa;

(vii) Kuacha kuchanganya nguruwe wageni na wenyeji kwenye banda moja; na

(viii) Wafugaji kutoa taarifa za ugonjwa au vifo vya nguruwe pindi inapojitokeza kwa mtaalamu wa mifugo aliye karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali kupitia Wizara ni kuendelea kutoa elimu ya udhibiti kwa wadau wote katika mnyororo wa thamani, wakiwemo wafanyabiashara na wasafirishaji wa nguruwe pamoja na watoa huduma za afya ya mifugo. Kazi hii tunaendelea kuifanya kwa kuzingatia uhalisia katika kila eneo kwa wafugaji wakubwa na wadogo.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza:-

Je, kwa nini mikopo ya injini za boti isitolewe kwa mtu mmoja mmoja aliye tayari kuliko kutoa kupitia vikundi jambo ambalo linachelewesha ukuaji wa Sekta ya Uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ibara ya 43(h) ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 – 2025 inaelekeza Serikali kuhamasisha uanzishaji na uimarishaji wa Vikundi na Vyama vya Ushirika vya Msingi vya Wavuvi Wadogo kwa lengo la kuwapatia mtaji, ujuzi na vifaa pamoja na zana za uvuvi katika maeneo ya mwambao wa bahari ya Hindi, Maziwa, Mabwawa na mito ili kuongeza uzalishaji, ajira na kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza ilani hiyo, kwa mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali iliazimia kuhamasisha wavuvi na wakuzaji viumbe maji kujiunga kwenye vyama vya ushirika ili kuwa na sauti ya pamoja, kufikiwa kirahisi, kutatua changamoto zinazowakabili pamoja na kuwa na usimamizi endelevu wa rasilimali za uvuvi. Aidha, Serikali imekuwa ikiviwezesha vyama vya ushirika kwa kuvipatia elimu, zana na vifaa bora vya uvuvi kama vile injini za boti pamoja na kuviunganisha na taasisi za kifedha ili kupata mikopo yenye riba na masharti nafuu kwa lengo la kufanya shughuli zao kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Serikali itaendelea kuhamasisha na kuwezesha vyama vya ushirika. Aidha, mtu mmoja mmoja anayo fursa ya kuomba kukopeshwa injini za boti kupitia taasisi za kifedha nchini. Hivyo, natoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote kuhimiza wavuvi na wakuzaji viumbe maji wa maeneo yenu kujiunga kwenye vyama vya ushirika vya wavuvi kama chachu ya kuwaletea maendeleo.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-

(a) Je, Serikali imejipanga vipi kupambana na tishio la uvuvi haramu nchini?

(b) Je, ni meli ngapi zilikamatwa nchini tokea mwaka 2015 - 2020 kwa kosa la uvuvi haramu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kupambana na tishio la uvuvi haramu, Serikali imeandaa Mkakati wa Ulinzi na Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi ambapo katika mpango huo ushirikishwaji wa jamii katika kusimamia na kulinda rasilimali za uvuvi kupitia Halmashauri, Serikali za Vijiji na Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi utaimarishwa. Aidha, kupitia mkakati huo, Serikali itaendelea kutoa elimu kuhusu athari za uvuvi haramu kwa mazingira, jamii na uchumi. Vilevile Serikali itaendelea kuimarisha Mashirikiano ya Kikanda na Kimataifa kwa kushirikiana na nchi mbalimbali zikiwemo Nchi za SADC katika kuzuia uvuvi haramu usioratibiwa na kuripotiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bahari Kuu, Serikali inao mfumo wa kufuatilia mienendo ya meli zote za uvuvi. Katika kipindi cha miaka mitano kuanzia 2015-2020, meli moja ya uvuvi haramu ilikamatwa Bahari Kuu na kufunguliwa mashtaka, ambapo Mahakama iliamuru mmiliki wa meli hiyo kulipa jumla ya shilingi bilioni moja au kufungwa jela miaka 20.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa uamuzi wa kuwaruhusu Wavuvi wa Kamba Koche kuvua kuanzia mwezi Desemba hadi Julai kila mwaka?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Meshimiwa Mweyekiti, kwa niaba wa Waziri ya Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Twaha Ally Mpembenwe Mbunge wa Kibiti kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003 pamoja na kanuni zake za Mwaka 2009 na Marekebisho yake ya mwaka 2020, Serikali haijawahi kuzuia uvuvi wa Kamba Koche au maarufu kama prawns. Hata hivyo, Serikali imeweka utaratibu kwa ajili ya uvuvi wa Kambamiti kwa wavuvi wadogo na wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uvuvi wa Kambamiti kwa mujibu wa Sheria na Kanuni zilizopo unaruhusiwa kufanyika kuanzia mwezi Machi hadi Septemba kila mwaka kwa ukanda wa Kaskazini unaohusisha Wilaya za Bagamoyo, Pangani Chalinze na kuanzia mwezi Aprili hadi Agosti kila mwaka kwa ukanda wa Kusini unaohusisha Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi kilichobaki kimeachwa ili Kambamiti kwa maana ya prawns waweze kuzaliana na kukua. Maamuzi haya yamefanyika baada ya taarifa za utafiti wa Kisayansi na kwa kuzingatia uendelevu wa Rasilimali hii.

Meshimiwa Mweyekiti, Serikali imekuwa ikisisitiza kwa wadau wote wa Uvuvi hususani Uvuvi wa Kambamiti yaana Prawns kufanya shughuli zao kwa mujibu wa Sheria na taratibu zilizopo kwa lengo la kuwa na uvuvi endelevu kwa maslahi mapana ya vizazi vilivyopo na vile vijavyo.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, upi ni mkakati wa Serikali wa kuendeleza Shamba la Mifugo la Kitulo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shamba la Kitulo ni miongoni mwa mashamba matano ya Serikali ya kuzalisha mifugo na ni shamba pekee linalozalisha ng’ombe aina ya Freisian halisi (pure). Mkakati uliopo ni wa miaka mitatu (2020/2021 – 2022/ 2023) ambao umelenga kuendeleza shamba kwa kuongeza ng’ombe wazazi kutoka 350 hadi 700, kununua madume ya ng’ombe wazazi 20, kuboresha malisho kwa kupanda malisho eneo la hekta 150, kuimarisha huduma ya uhimilishaji kufikia uhimilisha wa ng’ombe 300 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza mkakati huo, Wizara kupitia Bajeti ya Mwaka 2021/2022 imenunua madume matano ya ng’ombe wazazi kutoka shamba la Shafa Farm lililopo mkoani Iringa, kilo 400 za mbegu za malisho kutoka Marekani na kilo 100 kutoka Kenya kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa malisho. Aidha, shughuli nyingine ni uhimilishaji ambapo ng’ombe 135 wamehimilishwa na ununuzi wa tenki la kupoozea maziwa lenye ujazo wa lita 3,000 ambapo utaratibu wa manunuzi unakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, Shamba la Kitulo linahitaji uwekezaji wa kiasi cha shilingi bilioni 6.6 ili kufikia kiwango cha juu cha uzalishaji. Aidha, uwekezaji huu utaendelea kufanywa na Serikali kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE K.n.y. MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapima eneo la mifugo la Ruvu na kulikabidhi kwa Halmashauri ya Chalinze?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshapima na kutoa kipande cha ardhi chenye ukubwa wa hekta 2,208 kutoka Ranchi ya Ruvu kwa ajili ya matumizi ya wananchi. Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze ilikatiwa hekta 1,488 kwa ajili ya vijiji sita ambavyo ni Kijiji cha Ruvu Darajani hekta 200; Kijiji cha Kidogozero hekta 200; Kijiji cha Kitonga hekta 480; Kijiji cha Magulumatali hekta 200; Kijiji cha Vigwaza hekta nane; na Kijiji cha Milo-Kitongoji cha Kengeni hekta 400.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imepima na kutoa kipande cha ardhi chenye ukubwa wa hekta 120 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya vijiji vitatu vya Kidomole hekta 40; Fukayosi hekta 40 na Mkenge hekta 40. Pia, Serikali imepima na kutoa ardhi yenye ukubwa wa hekta 600 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Vijijini kwa ajili ya Kijiji cha Mperamumbi Kitongoji cha Waya.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH aliuliza:-

Je, Serikali itawasaidiaje Wafanyabiashara wa Dagaa wanaofuata Masoko nchi jirani ambao hutozwa ushuru Zanzibar na Tunduma kwa upande wa Tanzania Bara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mazao ya uvuvi yanayosafirishwa kwenda nje ya nchi au yanayoingizwa nchini kwa upande wa Tanzania Bara yanalipishwa ushuru stahiki wa Serikali kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Uvuvi pamoja na Sheria nyingine za Nchi. Aidha, dagaa wanaotoka Zanzibar kwenda nchi jirani kupitia mpaka wa Tunduma hawalipishwi ushuru wowote katika Bandari ya Dar es Salaam na wanapokuwa wamefikishwa Tunduma kuelekea nchi jirani.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka Maafisa katika Bandari ya Dar es Salaam na maeneo ya mipakani kwa ajili ya kudhibiti utoroshaji na biashara haramu ya mazao ya uvuvi nchini. Hata hivyo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuona umuhimu wa kulinda na kuendeleza rasilimali za uvuvi, itakutana na Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuangalia namna bora ya kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara wa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani katika kutatua changamoto zinazohusu masuala ya uvuvi.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza:-

Kwa kuwa wananchi wa Ludewa hutegemea Ziwa Nyasa kwa shughuli za uvuvi: -

(a) Je, Serikali haioni haja ya kupeleka mradi wa uhifadhi mazingira Ziwa Nyasa ili kutunza mazalia ya samaki ambao wameanza kuadimika?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka fedha pamoja na wataalam kutoa elimu ya kuanzisha mradi wa ufugaji samaki kwenye vizimba ndani ya Ziwa Nyasa ili kuzalisha ajira kwa wananchi na kuongeza kipato?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Ludewa lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara katika kutekeleza jukumu la kulinda, kusimamia, kuhifadhi na kuendeleza rasilimali za uvuvi nchini imekuwa ikitoa elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira kote nchini ikiwemo Ziwa Nyasa. Aidha, kwa sasa Serikali ipo katika hatua za mwisho za kuandaa mpango kabambe wa kuendeleza sekta ya uvuvi ambao utakapokamilika unatarajiwa kubainisha miradi ya uvuvi itakayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa mafunzo katika tasnia ya ukuzaji viumbe maji kwa kutumia teknolojia mbalimbali ikiwemo teknolojia ya vizimba, imetoa mafunzo ya vitendo kwa wananchi 1,885 kuhusu mbinu bora za ufugaji samaki, kilimo cha mwani na uongezaji thamani zao la mwani.

Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepanga kutoa mafunzo kwa wakuzaji viumbe maji wapatao 3,000 kote nchini wakiwemo wafugaji wa samaki Ziwa Nyasa kupitia Kituo cha Kuendeleza Ukuzaji Viumbe Maji cha Ruhila – Songea.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakuja na Mpango Madhubuti wa kuitumia Bahari kwa Programu za Uvuvi wa Bahari Kuu na michezo ya bahari ili kutengeneza ajira kwa Vijana wa Jimbo la Kawe, hasa ikizingatiwa nusu ya Jimbo hilo lipo Mwambao wa Bahari ya Hindi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Askofu Josephat Mathias Gwajima, Mbunge wa Kawe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na juhudi za kuimarisha uvuvi wa bahari kuu kwa kufufua Shirika la Uvuvi Tanzania, TAFICO ili kuiwezesha nchi kunufaika na rasilimali za uvuvi. Hususani zile zilizopo katika ukanda wa uchumi wa bahari kuu na bahari ya ndani. Hadi sasa Serikali ina mpango wa kununua meli tano za uvuvi, ambazo zitavua katika maji ya Kitaifa, Bahari kuu pamoja na kutoa leseni kwa meli kubwa zinazomilikiwa na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga bandari ya uvuvi katika ukanda wa pwani ya Bahari ya Hindi. Ambapo uwepo wa bandari hiyo, utawezesha meli za uvuvi zinazovua katika ukanda wa uchumi wa bahari ya Tanzania na bahari kuu kutia nanga, kushusha mazao ya uvuvi na kupata huduma mbalimbali, zikiwemo mafuta na chakula ambapo meli hizo zitachangia kutoa ajira kwa wananchi wakiwemo wa Jimbo la Kawe.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuboresha mazingira na usalama katika fukwe na visiwa vya Bahari ya Hindi, ili kuwavutia wawekezaji kuwekeza katika shughuli mbalimbali za michezo katika fukwe na visiwa hivyo.
MHE. SYLIVIA F. SIGULA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wavuvi wa Ziwa Tanganyika wavue kisasa ili kupata kipato zaidi na kutoa ajira kwa vijana?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiaw Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Sylivia Francis Sigula, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika juhudi za kusaidia na kuwezesha wavuvi wadogo kuvua kisasa, Serikali imerahisisha utaratibu wa kupata zana za kisasa za uvuvi. Serikali imefuta Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye vifaa vingi vya uvuvi ikiwemo engine za kupachika, nyuzi za kushonea nyavu, nyavu za uvuvi na vifungashio kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2011 na Sheria ya Mamlaka ya Mapato ya mwaka
2014 ili kuwasaidia wavuvi kupata zana za uvuvi kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vilevile, Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ili wavuvi wapate mikopo ya masharti na riba nafuu kutoka katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwa maana TIB. Aidha, Wizara kupitia Dawati la Sekta Binafsi imeviunganisha vyama vya ushirika vya wavuvi na taasisi za fedha ambapo mikopo iliyoombwa na kupitishwa ni shilingi bilioni 2.6 na mikopo iliyotolewa ni shilingi milioni 560.7. Pia Wizara imehamasisha Benki ya Posta kuanzisha na kuzindua Akaunti ya Wavuvi kwa ajili ya mikopo na bima mahususi kwa wavuvi hususan wavuvi wadogo.
MHE. YAHYA A. MHATA aliuliza:-

Je, wananchi wa Jimbo la Nanyumbu watanufaika vipi na Shamba la Uzalishaji Mifugo Nangaramo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Yahya Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shamba la Nangaramo ni miongoni mwa mashamba matano ya kuzalisha mitamba chotara wa maziwa na nyama kwa lengo la kusambaza kwa wafugaji.

Mheshimiwa Spika, faida zinazopatikana kwa wananchi wanaozunguka Shamba la Nangaramo ni pamoja na wananchi kupata elimu kupitia mikutano ya ujirani mwema kuhusu fursa za upatikanaji wa mitamba ya maziwa na nyama kwa lengo la kuwahamasisha kufuga ili kuboresha lishe ya familia, kutoa ajira na mbolea kwa uzalishaji wa mazao.

Mheshimiwa Spika, mbili, kutoa mafunzo ya ufugaji bora kwa shule za msingi na sekondari. Aidha, wanafunzi kutoka katika Shule ya Sekondari Mkangaula wamenufaika na mafunzo hayo walipokuwa kwenye mafunzo maalum; na tatu, uongozi wa shamba hushiriki shughuli mbalimbali za kijamii kama vile ujenzi wa shule na utoaji wa ajira za muda mfupi na mrefu kwa wananchi.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Bandari ya Uvuvi na kununua Meli ya uvuvi katika Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge wa Mtwara Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uvuvi ya Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 – 2025 Ibara 43(a) ambazo zimeainisha kujenga Bandari ya Uvuvi katika Ukanda wa Pwani ambayo itawezesha meli zinazovua Bahari Kuu kutia nanga kwa lengo la kushusha samaki na mazao ya uvuvi, kuuza samaki, kutoa takwimu sahihi na huduma nyinginezo ikiwemo kujaza mafuta, vyakula na matengenezo madogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutekeleza Mpango huo, Serikali iliingia mkataba na mshauri elekezi ili kubaini eneo linalofaa kwa ujenzi wa bandari. Baada ya uchambuzi huo, mshauri elekezi alipendekeza bandari ijengwe katika eneo la Mbegani – Bagamoyo, na kazi hiyo itaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na mahitaji na uwepo wa bajeti Serikali itaendelea kutazama uwezekano wa kujenga Bandari za Uvuvi katika maeneo mengine ikiwemo Mkoa wa Mtwara kwa siku za usoni ikiwa ni pamoja na kuboresha mialo, kuimarisha vikundi wa usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi na kuanzisha Vyama Vya Ushirika wa Wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwekezaji na ujenzi wa Bandari za Uvuvi utawezesha kukua kwa biashara na shughuli za uvuvi Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi ikiwemo Mkoa wa Mtwara.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza: -

(a) Je, ni asilimia ngapi ya mapato yatokanayo na Uvuvi wa Bahari Kuu yanaenda upande wa Zanzibar?

(b) Je, kwa miaka mitano iliyopita Zanzibar imepata kiasi gani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, mgawanyo wa mapato yatokanayo na uvuvi wa Bahari Kuu unafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu Na. 5 ya mwaka 2020, Kifungu cha 79, ambayo inaelekeza mgawanyo wa mapato yanayokusanywa na Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu kwa utaratibu ufuatao, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar asilimia 20; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania asilimia 30; na Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi Bahari Kuu asilimia 50.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu ilikusanya jumla ya Dola za Kimarekani 1,352,107.50 sawa na Sh.3,091,837,178.10. Kutokana na makusanyo hayo na kwa kuzingatia maelezo yangu katika kipengele (a), Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufikia mwezi Machi, 2021 imepata mgao wa Sh.618,367,435.62.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa majosho katika Wilaya ya Igunga, hususan Jimbo la Manonga?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Igunga ina jumla ya majosho 20. Kati ya hayo majosho 12 yanafanyakazi na majosho nane ni mabovu na hayafanyi kazi na hivyo kuhitaji ukarabati.

Aidha, halmashauri hiyo inahitaji jumla ya majosho 36 na hivyo ina upungufu wa majosho mapya 16 yanayohitajika kujengwa. Kati ya majosho mabovu nane, majosho matatu yanakarabatiwa na josho jipya moja linajengwa na halmashauri yenyewe kwa kutumia vyanzo vyake vya fedha za ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 jumla ya majosho 10 yatajengwa katika Halmashauri ya Igunga yakiwemo majosho matatu katika Jimbo la Manonga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ili kukabiliana na upungufu wa majosho, Halmashauri ya Igunga inashauriwa kuendelea kutenga asilimia 15 ya fedha inayokusanywa kutokana na mifugo kwa ajili ya kujenga na kukarabati majosho.
MHE. MWANTUM M. ZODO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya Wavuvi wa ukanda wa Pwani ili kuchochea uchumi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantum Mzamili Zodo, Mbunge - Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kuboresha mazingira ya wavuvi wa Ukanda wa Pwani, Serikali inafanya yafuatayo: -

(i) Serikali imeweka mazingira rafiki kwa wavuvi kupata mikopo ya masharti nafuu kutoka taasisi mbalimbali za fedha;

(ii) Kupitia ufadhili wa Shirika la IFAD, Serikali inaboresha masoko ya mazao ya uvuvi pamoja na kuweka miundombinu wezeshi ya kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi na;

(iii) Kupitia Taasisi ya Utafiti a Uvuvi (TAFIR), Serikali inatarajia kuweka vifaa vya kuvutia samaki katika Bahari ya Hindi kwa ajili ya kusaidia wavuvi kupata samaki kwa urahisi.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali inaendelea na programu ya kuainisha maeneo yenye uvuvi wenye tija kwa kutumia satellite ili kuwataarifu wavuvi maeneo ambayo samaki wanapatikana kwa wingi, ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza: -

Je, Serikali imesaidia mikopo kwa vikundi vingapi vya wavuvi Wilaya ya Nkasi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 – 2025 Ibara ya 43(h) inaelekeza Serikali ihamasishe uanzishaji na uimarishaji wa vikundi na Vyama vya Ushirika vya Msingi vya Wavuvi wadogo kwa lengo la kuwapatia mitaji, ujuzi na vifaa pamoja na zana za uvuvi. Katika kutekeleza ahadi hiyo, Serikali imefanya yafuatayo: -

(a) Imeendelea kuhamasisha wavuvi kujiunga kwenye Vyama vya Ushirika vya Wavuvi ambapo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 jumla ya wadau 16,733 kutoka halmashauri 21 nchini wamepatiwa mafunzo hayo ikiwemo halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ambapo hadi sasa jumla ya Vyama vya Ushirika 146 vya Wavuvi vimeundwa.

(b) Serikali imeendelea kuwezesha wavuvi kupitia Vyama vya Ushirika vya Wavuvi kwa kuvipatia injini za boti, ambapo kwa sasa Serikali ipo kwenye mchakato wa kuvipatia injini za kupachika Vyama vya Ushirika vya Wavuvi kumi kikiwemo Chama cha Ushirika Kabwe kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, ahsante.
MHE. NORA W. MZERU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wafugaji wa Mkoa wa Morogoro kufanya ufugaji wa kisasa na wenye tija kwa kuwa Mkoa huu una wafugaji wengi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nora Waziri Mzeru Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali, ili kufanya ufugaji katika Mkoa wa Morogoro kuwa wenye tija na wa kisasa. Juhudi hizo ni pamoja na uboreshaji wa mbari za mifugo kwa kuhimilisha ngómbe, kuwezesha upatikanaji wa kuku wazazi walioboreshwa, mafunzo rejea juu ya teknolojia za ufugaji bora kwa wafugaji na maafisa ugani. Vipindi vya elimu kwa umma vya redio, televisheni, maonyesho mbalimbali yakiwemo ya sabasaba na nanenane.

Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi hizi, hadi mwaka 2020 mifugo iliyoboreshwa katika Mkoa wa Morogoro imefikia ng’ombe 28,582 sawa na asilimia 3 ya ng’ombe wote na mbuzi 19,899 sawa na asilimia 11 ya mbuzi wote na kuku millioni 2.5 sawa na asilimia 69 ya kuku wote.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2021/2022 Wizara kwa kushirikiana na wadau na Mamlaka za Serikali za Mitaa, inatarajia kuhimilisha ng’ombe 32,606 Mkoani Morogoro, kwa kutumia mbegu bora za mifugo za ruzuku kutoka katika Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji cha NAIC Arusha. Ahsante sana.
MHE. VINCENT P. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga masoko ya samaki katika Ukanda wa Ziwa Tanganyika hususani Kata ya Kala Mpasa, Wampambe, Kizimbi na Naninde ili wavuvi wapate maeneo ya kuuzia samaki badala ya kulazimika kwenda kuuza nchi za jirani za Zambia, Congo na Burundi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga miundombinu ya uvuvi katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika mwambao wa Ziwa Tanganyika. Miundombinu ya Mialo na Masoko ni muhimu katika kuhakikisha kuwa na mazao bora na salama, kupunguza upotevu wa mazao na kusaidia ukusanyaji wa taarifa na mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na umuhimu huu, ujenzi wa masoko unahitaji rasilimali ikiwemo ardhi na fedha. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali ipo tayari kujenga Soko, katika Wilaya ya Nkasi kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, namuomba Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kuandaa eneo katika Wilaya ya Nkasi, ili kuwezesha hatua za ujenzi wa soko kuanza pindi fedha itakapopatikana. Ahsante.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Benki ya Wavuvi nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kwamba Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) tayari ipo kwa ajili ya kutoa huduma za kifedha kwa wadau wa sekta za kilimo, mifugo na uvuvi. Benki hii ilianzishwa mnamo mwezi Septemba, 2012 chini ya Sheria ya Makampuni (Sura ya 212).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilianzisha Benki hiyo ili kusaidia kuongoza mageuzi ya kuleta maendeleo kwenye sekta ya kilimo sambamba na kujenga uwezo wa wadau kutekeleza programu mbalimbali za kuongeza thamani mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. Benki hii inatoa mikopo ya muda mfupi, wa kati na mrefu kwa watu binafsi na vikundi vinavyojishughulisha na sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumshauri Mheshimiwa Mbunge awahamasishe wavuvi kuchangamkia fursa mbalimbali za mikopo na huduma nyinginezo za kifedha zinazotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Ahsante.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha Miundombinu ya Minada ya Mifugo kwa kujenga mazizi ya kisasa, vyoo na ofisi za kupokea tozo na kodi za mnada?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Steven Lemomo Kiruswa - Mbunge wa Longido kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha minada nchini ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wizara katika bajeti ya maendeleo imetenga kiasi cha Shilingi Bilioni 4.46 kwa ajili ya kukarabati na kujenga miundombinu ya minada 19 ya upili mpakani na ya awali kwa kujenga uzio, ofisi, mazizi ya kisasa ya ng’ombe na mbuzi, vyoo, vipakilio na mabirika ya kunywea maji mifugo katika minada ya Pugu (Dar es Salaam), Mkiu (Pwani), Mtukula (Kagera), Horohoro (Tanga), Ndelema (Tanga), Malampaka (Simiyu), Magena (Mara), Igunga-(Tabora), Buhigwe (Kigoma), Ipuli (Tabora), Wasso (Arusha), Gendi (Manyara), Kileo (Kilimanjaro), Meserani (Arusha), Nyanguge (Mwanza), na Nyamatala (Mwanza). Utekelezaji unatarajiwa kuanza mwezi huu wa Novemba, 2021 na utachukua miezi minne kukamilika.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya minada nchini kulingana na uwezo wa kibajeti. Ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga masoko ya kisasa ya kuuzia samaki hasa katika Kata ya Somanga na Kivinje ambazo upatikanaji wa samaki ni mkubwa ili kuboresha maisha ya wavuvi wa Wilaya ya Kilwa kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kasmazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa Kata ya Somanga na Kata ya Kivinje ni miongoni mwa maeneo yenye samaki wengi katika Wilaya ya Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 kupitia mradi wa IFAD imetenga fedha kiasi cha shilingi 211,698,940 kwa ajili ya ujenzi wa mitambo ya kuzalisha barafu. Wilaya ya Kilwa ni moja ya maeneo ambayo mitambo ya kuzalisha barafu itajengwa ili kusaidia kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutekeleza mipango ya kuboresha miundombinu ya uvuvi, ikiwemo masoko ya kisasa ya uvuvi katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwa ni pamoja na Kata ya Somanga na Kivinje katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kadri fedha zinavyopatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO aliuliza: -

Je, ni Ranchi ngapi nchini zimeshawapokea wafugaji na kuwapatia nafasi ya kufuga kwenye Ranchi hizo kama Serikali ilivyotoa maelekezo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Costantino Mwakamo Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) imetekeleza maelekezo ya Serikali kwa kutenga jumla ya vitalu vya muda mrefu 116 katika Ranchi 11 za NARCO na kuzikodisha kwa wafugaji wadogo 116. Ranchi hizo ni Kikulula (Kagera) vitalu 2, Mabale (Kagera) vitalu 7, Kagoma (Kagera) vitalu 18, Kitengule (Kagera) vitalu 10, Missenyi (Kagera) vitalu 11, Mkata (Morogoro) vitalu 7, Dakawa (Morogoro) vitalu 2, Mzeri Hill (Tanga) vitalu 9, Usangu (Mbeya) vitalu 16, Kalambo (Rukwa) vitalu 13 na Uvinza (Kigoma) vitalu 21. Jumla ya eneo la vitalu hivi ni hekta 322,525.

Mheshimiwa Spika, katika juhudi za kutatua migogoro ya wakulima, wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi nchini hasa baada ya wafugaji kuondolewa kwenye hifadhi za misitu na mapori ya akiba, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) ilianzisha utaratibu wa kugawa vitalu vya muda mfupi ambapo jumla ya vitalu 128 vimekodishwa kwa wafugaji wadogo 128 kutoka katika Ranchi 10 za NARCO. Ahsante sana.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapatia wavuvi elimu ya uelewa kuhusu madhara ya uvuvi haramu ili wasifanye aina hiyo ya uvuvi na kuharibu mazingira ya maziwa na bahari nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii ya kujibu maswali, lakini kwanza naomba nami nimshukuru Mwenyezi Mungu; na pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini katika Wizara hii kwa nafasi hii ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo ya shukrani, naomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakubaliana kabisa na Mheshimiwa Mbunge kuwa ni muhimu sana kuwapatia wavuvi elimu kuhusu madhara ya uvuvi haramu ili wasifanye uvuvi haramu na tuweze kulinda rasilimali za uvuvi nchini. Katika kutekeleza jukumu hili, Serikali imekuwa ikitoa elimu hiyo kupitia vipindi vya redio, runinga, mikutano, vipeperushi, semina na maonesho mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wataalam wa Wizara wamekuwa wakitoa elimu kwa kuwafikia wavuvi na wadau wengine moja kwa moja katika maeneo yao ambapo kwa mwaka 2021/2022 mikoa ambayo tayari imefikiwa ni mikoa ya Tanga, Pwani, Mwanza, Mara, Kagera na Katavi. Ahsante sana.
MHE. YUSTINA A. RAHHI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuchimba malambo kwa ajili ya maji ya mifugo katika maeneo ya wafugaji mkoani Manyara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/ 2021, Serikali imekamilisha ukarabati wa mabwawa matatu likiwemo bwawa la Narakauo lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itaendelea kutenga fedha za kuchimba mabwawa na visima virefu katika maeneo mbalimbali nchini hususan maeneo yaliyoathirika na ukame ukiwemo Mkoa wa Manyara.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuhimiza Mamlaka zote za Serikali za Mitaa nchini kutekeleza Waraka wa Rais Na.1 wa Mwaka 2002, unaozielekeza kutenga fedha kiasi kisichopungua asilimia 15 kwa mapato yatokanayo na mifugo ili zitumike kutekeleza shughuli za Sekta ya Mifugo ikiwemo uchimbaji na ujenzi wa miundombinu ya maji kwa ajili ya mifugo. Aidha, Uboreshaji wa miundombinu hiyo ya mifugo uwe Shirikishi kwa kuwahusisha wafugaji.
MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Bwawa la Zombo linatumika kikamilifu kwa ufugaji wa samaki na kuondoa tatizo la ajira kwa vijana?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa ina mpango endelevu wa kufanya tathmini ya mabwawa yaliyopo katika halmashauri mbalimbali nchini ili kufahamu uwekezaji unaofaa kwenye bwawa husika kulingana na jiografia ya eneo hilo. Kwa kuwa shughuli hii ni endelevu na hufanyika kwa awamu, Bwawa la Zombo litaingia kwenye mpango wa tathmini katika mwaka wa fedha 2022/2023 ili kujua aina ya uwekezaji unaofaa katika Bwawa hilo.

Mheshimiwa Spika, vile vile, wataalam wa Kituo cha Ukuzaji Viumbe Maji cha Kingolwira – Morogoro watatoa mafunzo maalum ya ufugaji samaki kwa vijana wa Jimbo la Mikumi ili kuwapa stadi za ufugaji samaki wenye tija kwenye mabwawa kwa lengo la kutengeneza ajira. ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mialo katika Forodha za Nankanga na Ilanga zilizopo ndani ya Ziwa Rukwa ili kurahisisha shughuli za Uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Kwela, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango mkakati wa Serikali ni kuhakikisha inajenga na kuboresha mialo katika maeneo mbalimbali nchini yanayojishughulisha na shughuli za uvuvi ikiwemo maeneo yanayozunguka Ziwa Rukwa kama vile forodha za Nankanga na Forodha ya Ilanga. Aidha, utekelezaji wa mkakati huu unategemea upatikanaji wa rasilimali fedha.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italirejesha Shamba la kupumzishia Mifugo la Kinyangiri kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Iramba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia umuhimu wa maeneo haya katika biashara ya mifugo na mazao yake, hususan kipindi hiki ambapo soko la nyama limezidi kuongezeka nje ya nchi, Serikali inakusudia kuendelea kuboresha maeneo yake yote ya mifugo ikiwa ni pamoja na eneo la Kinyangili ili kusudi biashara ya mifugo na biashara ya nyama nchini iweze kushamiri kwa kuzingatia viwango vyote vinavyotakiwa katika Soko la Kitaifa na Kimataifa. Ahsante. (Makofi)
MHE. KENNETH E. NOLLO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo cha uzalishaji wa madume bora ya ng’ombe Wilayani Bahi ili kuleta tija kwa wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Ernest Nollo, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kuimarisha mashamba yake ya uzalishaji wa madume bora ya Mabuki, Mwanza; Kitulo, Njombe; na Sao Hill lililopo Mkoani Iringa ili yaweze kuzalisha madume mengi na bora kwa lengo la kuyasambaza kwa wafugaji wote wanaohitaji ikiwa ni pamoja na wafugaji wa Wilaya ya Bahi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali inaendelea kusisitiza matumizi ya teknolojia ya uhimilishaji katika kuboresha kosaafu za ng’ombe ili kuwa na kundi la mifugo yenye tija katika kuzalishaji nyama na maziwa na hivyo kukidhi mahitaji ya soko.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza: -

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhusu mpango wa kukuza uchumi wa buluu kwa kuzingatia mazao yatokanayo na bahari?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kukuza uchumi wa buluu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi chini ya uratibu wa Ofisi ya Makamu wa Rais na kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo, mashirika ya kijamii, na sekta binafsi tunaandaa Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Buluu. Mazao ambayo yamepewa kipaumbele kwenye mkakati huo kwa upande wa baharini ni samaki aina ya dagaa, pweza, kambamiti, vibua, jodari, changudoa, zao la mwani, unenepeshaji wa kaa na ukuzaji wa lulu.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 11.51 ambazo zitatumika kununua boti za kisasa zenye engine, kifaa cha kutafutia samaki (GPS) na kasha la ubaridi lenye uwezo wa kubeba tani 1.5 kwa ajili ya kuwakopesha wavuvi. Pia jumla ya shilingi bilioni 20 zimetengwa ambapo kiasi cha shilingi bilioni 3.32 zitatumika kuwezesha pembejeo kwa ajili ya wakulima wa mwani katika ukanda wa bahari ya Hindi. Ahsante.
MHE. TABASAM H. MWAGAO aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa banda la ukaguzi na kupokea samaki wabichi katika Kata ya Chifunfu utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabasam Hamis Mwagao, Mbunge wa Sengerema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa banda la kupokelea samaki Chifunfu uliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema ulianza mwezi Mei, 2021 chini ya Mkandarasi M/S Fast Construction Company Limited ya Mkoani Mwanza kwa thamani ya shilingi 124,592,064.00 ambapo hadi sasa ujenzi umefikia hatua ya kuezeka na Mkandarasi ameshalipwa kiasi cha shilingi 95,768,193.00.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya ujenzi wa banda hilo ilipangwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi sita, hata hivyo Mkandarasi hakuweza kukamilisha kazi hiyo kwa mujibu wa mkataba, hivyo Serikali imechukua hatua za kusitisha Mkataba wa Mkandarasi huyo na hatua zingine za kisheria zinaendelea dhidi yake.
MHE. YAHYA ABDULWAKIL AHMED aliuliza: -

Je, ni lini ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ununuzi wa meli nane za uvuvi itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI aljibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Abdulwakil Ahmed, Mbunge wa Kwahani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali, naomba nifanye maboresho madogo sana katika aya inayosema katika mwaka wa fedha 2023/2024, badala yake isomeke katika mwaka wa fedha 2022/2023 Mheshimiwa Spika, baada ya maboresho hayo, naomba niendelee sasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea na hatua mbalimbali za ununuzi wa meli nane (8) za Uvuvi katika Bahari Kuu kama alivyoagiza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza agizo hilo Serikali itanunua meli nane kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) chini ya Mfuko wa Kimataifa wa Kuendeleza Kilimo-IFAD kwa awamu mbili ambapo katika mwaka wa fedha 2023/2024, meli nne na vifaa vyake zitanunuliwa. Meli hizo zitagawanywa Tanzania Bara meli na Zanzibar meli.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Mkataba baina ya Serikali na IFAD ununuzi wa meli hizo unatakiwa kukamilika baada ya kufanyika kwa tathmini ya athari za kimazingira na kijamii pamoja upembuzi wa kina wa uendeshaji wa meli za uvuvi. Hata hivyo, taratibu za kufanya Upembuzi huu yakinifu zinaendelea. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza mchakato wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi katika Mji wa Kilwa Masoko?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza ujenzi wa Bandari ya Uvuvi katika eneo la Kilwa Masoko Mkoani Lindi. Mkataba wa ujenzi wa Bandari hiyo ulisainiwa tarehe 07 Juni, 2022 kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Mkandarasi ambaye ni Kampuni ya M/S China Harbour Engineering. Aidha, maandalizi ya awali ya ujenzi wa Bandari hiyo yameanza na ujenzi unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 24. Ahsante.
MHE. STELLA S. FIYAO aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kuzuia nyavu haramu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara imeandaa Mkakati wa Kusimamia Rasilimali za Uvuvi ambao unajumuisha mbinu mbalimbali za kudhibiti utengenezaji, uagizaji, matumizi na biashara ya nyavu haramu za uvuvi. Utekelezaji wa mkakati huo unahusisha wadau mbalimbali ikiwemo vyombo vya ulinzi na usalama, sheria, watendaji wa taasisi zilizopo mipakani, bandarini na viwanja vya ndege; Viongozi wa Mikoa na Wilaya, wavuvi pamoja na watendaji wa Wizara kupitia vituo vya ulinzi wa rasilimali za uvuvi. Aidha, elimu kwa wadau kuhusu matumizi ya nyavu sahihi, uvuvi endelevu na wenye tija inaendelea kutolewa. Ahsante.
MHE. REGINA N. QWARAY aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuchimba mabwawa ya kuhifadhia maji kwa ajili ya kunyweshea mifugo katika kila Kijiji nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha maeneo yenye mifugo mingi na yale yaliyoathirika na ukame mara kwa mara yanakuwa na miundombinu ya maji yakiwemo mabwawa kwa ajili ya maji ya mifugo. Katika kutekeleza mkakati huo, mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni 2.146 kwa ajili ya uchimbaji na ujenzi wa mabwawa au malambo na visima virefu vya maji kwa ajili ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga fedha za kuchimba, kujenga na kukarabati mabwawa ama malambo na visima virefu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, napenda kutoa wito kwa Halmashauri za Wilaya, wafugaji na wadau wengine kuchimba na kujenga malambo au mabwawa, visima virefu kwa ajili ya maji ya mifugo. Pia, nahimiza wafugaji kuwa na vyanzo vyao binafsi vya maji kwa ajili ya mifugo yao.
MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza: -

Je, Serikali ina kauli gani juu ya ushuru mkubwa wa bidhaa za ngozi unaotozwa bandarini na vikwazo vya kusafirisha bidhaa hiyo nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango vya ushuru wa kusafirisha ngozi ghafi na ngozi iliyosindikwa kiwango cha kati kwa maana ya Wet blue nje ya nchi ni makubaliano ya Nchi Wanachama za Jumuiya ya Afrika Mashariki waliokubaliana kuainisha viwango vya ushuru kwa lengo la kuhakikisha viwanda vya ndani vinapata malighafi ya kutosha na kuzalisha bidhaa za ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushuru wa kusafirisha ngozi ghafi nje ya nchi kwa maana export levy ni asilimia 80 ya mzigo ukiwa bandarini kwa maana FOB au Dola za kimarekani 0.52 kwa kilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ngozi zilizosindikwa kwa kiwango cha kati kwa maana ya Wet blue zinatozwa ushuru wa asilimia 10 ya FOB ili kutoa motisha kwa wasindikaji. Ngozi zilizosindikwa hadi kufikia hatua ya mwisho kwa maana ya finished leather hazitozwi ushuru wowote ule, ni 0%. Jitihada hizo zimesaidia kuvutia uwekezaji katika viwanda vya kusindika ngozi na kuzalisha bidhaa za ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna vikwazo vyovyote katika kusafirisha zao la ngozi, kwa kuwa takwimu zinaonyesha kiwango cha usafirishaji wa ngozi ghafi kimeendelea kupanda kutoka kilo 513,201 mwaka 2015/2016 hadi kufikia kilo 7,370,533 mwaka 2020/2021.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kuwapatia vifaa vya kisasa wananchi wanaofanya shughuli za kukausha dagaa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inatarajia kujenga vichanja 80 vya kukaushia dagaa (drying racks), kununua mitambo minne ya umeme ya kukaushia dagaa (electric drier) na Solar Tents 15 katika Halmashauri za Kilwa, Mafia, Pangani na Bagamoyo katika mwaka wa fedha 2023/2024. Pia Wizara itaendelea kuwahamasisha na kuwaunganisha Wajasiriamali wa Sekta ya Uvuvi ili waweze kupata mikopo nafuu kupitia TADB itakayowawezesha kununua zana bora na za kisasa za kuendesha uvuvi endelevu, biashara yenye tija ya mazao ya uvuvi na matumizi ya vifaa vya kisasa vya kukaushia dagaa.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga josho katika Kata ya Miula Wilayani Nkasi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI aljibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Wizara ilipeleka kiasi cha shilingi milioni 108 kwa ajili ya ujenzi wa majosho sita katika Hamashauri ya Nkasi katika Vijiji vya Kipande, Katani, Chala, Mikukwe, Chalatila na Sintali. Majosho hayo yapo katika hatua mbalimbali za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kuwasiliana na Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi ili kukamilisha ujenzi wa majosho hayo na kutoa fursa kwa Serikali kutenga fedha zaidi kwa ajili ya ujenzi wa majosho mengine Nkasi Kusini ikiwemo Kata ya Miula. Aidha, Serikali inaendelea kuhamasisha wafugaji kuchangia ujenzi wa miundombinu ya mifugo ikiwemo majosho katika maeneo yao. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: -

Je, ni kiasi gani cha ngozi kinazalishwa kwa mwaka mzima na kutumika nchini na kiasi gani ghafi kinauzwa nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Josepha Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inazalisha wastani wa vipande milioni 13.6 vya ngozi kwa mwaka. Kati ya vipande hivyo, milioni 4.2 ni vya ng’ombe, vipande milioni 6.9 ni vya mbuzi na vipande milioni 2.5 ni vya kondoo. Kwa sasa, tunavyo viwanda vitatu vinavyofanya kazi ya usindikaji wa ngozi katika hatua ya kati (wet blue) na hatua ya mwisho (finished leather).

Mheshimiwa Naibu Spika, ngozi zinazosindikwa katika hatua ya kati ni vipande 51,866 vya ngozi ya ng’ombe na vipande 262,229 vya mbuzi na kondoo. Usindikaji hadi hatua ya mwisho ni vipande 145,000 vya ngozi ya ng’ombe na vipande 259,000 vya ngozi ya mbuzi na kondoo. Pia, kuna wasindikaji wadogo wanaosindika na kutengeneza bidhaa za ngozi maeneo mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inauza nje ya nchi ngozi ghafi na iliyosindikwa hatua ya awali, wastani wa vipande 1,630,740 vyenye thamani ya Shilingi Bilioni 10.5 kwa mwaka. Ngozi hiyo, inauzwa katika nchi za Nigeria, Afrika ya Kusini, Ghana, Togo, Pakistan, Marekani, Italia, Dubai na China, ahsante sana.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza:-

Je, ni kwa kiwango gani task forces zimepunguza tatizo la uvuvi haramu katika Ziwa Victoria kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2017/2018 - 2019/2020, Kikosi Kazi kilifanya doria na operesheni katika maeneo mbalimbali ya Ukanda wa Ziwa Victoria. Utekelezaji wa doria hizo uliwezesha kukamatwa kwa zana haramu zilizokuwa zikitumika katika shughuli za uvuvi ikiwemo nyavu za makila, makokoro, nyavu za timba (monofilament) na nyavu za dagaa. Pia, vifaa vilivyokuwa vinatumika kwenye uvuvi haramu na utoroshaji wa mazao ya uvuvi ikiwemo injini pamoja na boti na magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa doria hizo katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria uliwezesha kupungua kwa vitendo vya uvuvi haramu, biashara ya samaki wachanga na utoroshaji wa mazao ya uvuvi kwenda nje ya nchi kwa asilimia takribani 80; ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga majosho ya kuogesha mifugo katika Halmashauri ya Msalala?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, (Mb), kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilifanya ukarabati wa majosho matano (5) katika kata za Burige, Lunguya, Mega, Ntobo na Ngaya zilizoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala. Aidha, Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa majosho katika halmashauri mbalimbali nchini; ikiwemo Halmashauri ya Msalala. Pia Serikali inaendelea kuhamasisha wafugaji kuchangia ujenzi wa miundombinu ya mifugo ikiwemo ujenzi wa majosho. Ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha Wakulima wa zao la Mwani ili kuongeza tija?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2022/2023 Serikali imetenga fedha za program maalum ya Shirika la Fedha Duniani (IMF) kupitia dirisha la Extended Credit Facility (ECF) kwa ajili ya kuwawezesha wakulima wa mwani pembejeo kwa mkopo wa masharti nafuu na usio na riba kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha kwa awamu ya kwanza, Wizara itatoa pembejeo za mwani zenye thamani ya shilingi 447,251,244 kwa wakulima 343 waliokwenye vikundi katika wilaya saba za Muheza, Pangani, Mtama, Mkuranga, Kilwa, Lindi Mjini na Mtwara Vijijini, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia vikundi vya Uvuvi katika Jimbo la Mtwara Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhamasisha wavuvi kuunda vyama vya ushirika pamoja na kuviunganisha na taasisi mbalimbali za fedha kwa ajili ya kupata mikopo ya kuboresha shughuli zao za uvuvi, kukuza uchumi wao binafsi na Taifa ambapo hadi sasa kuna jumla ya vyama vya ushirika 170 nchi nzima. Kati ya vyama hivyo, vitatu viko katika Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara imetoa mkopo wa shilingi milioni nane kwa Kikundi cha Uvuvi cha Kaza Moyo Mtwara kwa ajili ya kununua injini na nyavu. Aidha, kupitia mradi wa unaoratibiwa na Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi kwa maana ya FETA, ufadhili wa UNDP Kikundi cha NASARC cha Mtwara Mjini na Kikundi cha wanawake cha Umoja ni Nguvu na chenyewe ni cha Mtwara Vijijini, vimejengewa jumla ya mabwawa 13 ya kufugia samaki wa maji baridi. Jumla ya wanufaika wa mradi huu ni wananchi 140 kutoka katika Vijiji vya Msanga Mkuu, Kijiji cha Mtawanya, Msijute na Mikindani. Mradi huu una thamani ya bilioni moja. Vilevile mradi umelipia gharama zote muhimu za uzalishaji ikiwemo kununua vifaranga na chakula cha samaki hadi kuvuna.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: -

Je Serikali ina mkakati gani wa kushughulikia soko la ndani la maziwa kwa kuhimiza na kuhamasisha unywaji wa maziwa shuleni kabla ya kutafuta masoko ya nje?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Magessa Tumaini, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na mkakati wa kukuza soko la maziwa nchini kwa kuimarisha na kuendeleza programu mbalimbali zinazochochea unywaji wa maziwa ikiwemo programu ya unywaji wa maziwa shuleni. Mpango wa unywaji maziwa shuleni umeweza kuwafikia watoto 90,000 wa shule za msingi 39 katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Iringa, Mbeya, na Tanga.

Vilevile Serikali inaendelea kuhamasisha unywaji maziwa nchini, kwa kutoa elimu kupitia vyombo vya habari, maonesho mbalimbali ya Wiki ya Maziwa Kitaifa inayoadhimishwa mwezi Mei kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itakutana na wadau mbalimbali wakiwemo wa tasnia ya maziwa ili kuandaa mikakati thabiti kwa lengo la kuongeza idadi ya shule zinazotoa huduma ya unywaji wa maziwa. (Makofi)
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Chuo Kikuu cha Uvuvi na Usafirishaji baharini katika eneo la Kikwetu - Lindi ambapo tayari Ekari 150 zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Lindi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi haina mpango wa kujenga Chuo Kikuu cha Uvuvi katika eneo la Kikwetu Lindi Mjini. Hata hivyo, Serikali kupitia Chuo cha Taifa cha Usafirishaji kwa maana ya NIT imepewa eneo lenye ukubwa wa ekari 125 lililopo Kikwetu Lindi. Eneo hilo ambalo tayari NIT imekamilisha taratibu za kumiliki, litatumika kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Lindi ya Chuo cha Taifa cha Usafirishaji ambacho kitatoa kozi katika ngazi ya Astashahada, Stashahada na Shahada katika fani mbalimbali za usafirishaji na uchukuzi ikiwemo Utengenezaji wa meli, uendeshaji wa vyombo vya majini na huduma za bandari.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2022/2023 kazi zitakazofanyika katika eneo hilo ni kuandaa mpango kabambe wa matumizi bora ya ardhi katika eneo hilo. Sambamba na maelezo hayo, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba, Serikali kupitia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam inatarajia kujenga Kitivo cha Kilimo katika Halmashauri ya Lindi Mjini ambapo tayari wameomba kupatiwa hekta 500.

Mipango ya maandalizi ya ujenzi wa chuo hicho inaendelea kwa ushirikiano kati ya Mkoa wa Lindi, Halmashauri ya Lindi Mjini na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA K.n.y. MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kukomesha uvuvi haramu wa kuvua samaki kwa kutumia nyavu zenye matundu madogo?
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aleksia Asia Kamguna, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaboresha mfumo wa utoaji wa vibali vya kuingiza zana za uvuvi nchini ili kudhibiti uingizwaji wa zana haramu ikiwemo nyavu zenye matundu madogo na makokoro. Aidha, Serikali inaendelea kuimarisha shughuli za ukaguzi wa zana za uvuvi zinazoingizwa nchini kupitia njia za mipakani na bandarini kwa kuongeza idadi ya watumishi na vitendea kazi. Hili litaongeza wigo wa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo ya mipakani na bandarini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeandaa Mkakati wa muda mfupi na muda mrefu wa kudhiti vitendo vya uvuvi haramu nchini. Utekelezaji wa mkakati huo utashirikisha viongozi wa ngazi za Vijiji, Kata, Tarafa, Wilaya na Mikoa ili kudhibiti matumizi ya zana haramu ikiwemo nyavu zenye matundu madogo, kokoro na nyinginezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wavuvi, waingizaji na wasambazaji wa zana za uvuvi pamoja na jamii kwa ujumla kuhusu athari za matumizi ya zana haramu za uvuvi zikiwemo nyavu zenye matundu madogo, kokoro, timba, freemaya pamoja na matumizi ya vilipuzi katika uvuvi, ahsante.
MHE. AMOUR KHAMIS MBAROUK aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawaendeleza wavuvi kwa kuanzisha uvuvi unaotumia dira maalum inayoelekeza samaki walipo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amour Khamis Mbarouk, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (Tanzania Fisheries Research Institute - TAFIRI), imeshaanza kuteleleza mradi wa kutambua maeneo yenye samaki yanayofaa kwa uvuvi (Potential Fishing Zones - PFZs) katika Bahari ya Hindi ili kuwasaidia wavuvi kujua maeneo yenye samaki wengi. Aidha, katika mradi huu, wavuvi wanawezeshwa kufanya uvuvi unaotumia dira maalum kwa kupewa taarifa za kijiografia (GPS) kupitia simu za mkononi ili kujua maeneo yenye samaki kwa wakati husika. Mradi huu wa majaribio ulifanyika kwa mafanikio kwa kushirikiana na wavuvi wa maeneo ya Mafia na Tanga kwa upande wa Tanzania Bara na Unguja na Pemba kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa TAFIRI inatengeneza programu maalumu (mobile app) ambayo itawawezesha wavuvi kupata taarifa za maeneo ya uvuvi ambako samaki wanapatikana kwa wingi. Aidha, programu hiyo imekamilika kwa asilimia 90. Ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga soko la kisasa la mazao yatokanayo na uvuvi Wilayani Nkasi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI, alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kujenga na kuboresha miundombinu ya uvuvi ikiwemo mialo na masoko katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa upande wa mwambao wa Ziwa Tanganyika unaojumuisha Wilaya ya Nkasi shughuli za uvuvi zinafanyika katika mialo ipatayo 239. Kati ya mialo hiyo, Serikali iliboresha mialo minne ya Kibirizi, Ikola, Muyobozi na Kirando katika Wilaya ya Nkasi ambapo Mheshimiwa Mbunge anawakilisha. Aidha, Serikali imejenga na kuboresha masoko mawili ya samaki ya Kibirizi na Kasanga Wilayani Sumbawanga. Pia kwa sasa Serikali inaendelea na jitihada za kuupandisha hadhi mwalo wa Kirando uliopo Wilaya ya Nkasi ili uweze kufikia hadhi ya kuwa soko la kisasa la samaki na mazao ya uvuvi. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:-

Je, kuna mipango gani ya kuweka mazingira wezeshi ya kupata mbegu bora za malisho kama Luseni pamoja na kuwezesha uzalishaji wa mitamba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Josepha Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuimarisha mashamba yake ya kuzalisha mbegu za malisho kwa kuyapatia vitendea kazi na kuongeza ukubwa wa maeneo ya kuzalisha mbegu za malisho na malisho. Aidha, nitumie fursa hii kuendelea kuihamasisha sekta binafsi kuwekeza katika uzalishaji wa mbegu za malisho na malisho kibiashara ili kukidhi mahitaji ya ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha uzalishaji wa mitamba, mpango wa Serikali ni kuendelea kuyaimarisha mashamba yake ya kuzalisha mitamba ya kituo cha kuzalisha mbegu za mifugo kwa ajili ya uhimilishaji cha NAIC- Arusha ili kuzalisha na kusambaza mitamba na mbegu bora za ng’ombe kwa gharama nafuu.
MHE. MOHAMED SAID ISSA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kuhamasisha kilimo cha zao la Mwani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Said Issa, Mbunge wa Jimbo la Konde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilishaanza kuhamasisha na kutoa elimu kuhusu zao la mwani na tayari jumla ya wakulima 4,569 wamepatiwa mafunzo ya uzalishaji, uhifadhi na kuongeza thamani katika zao la mwani. Ahsante sana.