Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Eng. Gerson Hosea Lwenge (19 total)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-
Mkoa wa Ruvuma una jumla ya Wilaya sita zenye Majimbo tisa ya uchaguzi, unakabiliwa na tatizo kubwa la maji:-
Je, ni lini Serikali itapeleka maji safi na salama katika Mkoa wa Ruvuma?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa utekelezaji wa miradi ya maji vijijini ulioanza mwaka wa fedha 2006/2007, Mkoa wa Ruvuma ulipangiwa vijiji 80. Kati ya vijiji hivyo, vijiji 76 vilipata vyanzo vya maji na Vijiji vinne vya Mchoteka, Nakapanya, Mtina na Muhuwesi katika Halmashauri ya Tunduru vilikosa vyanzo. Miradi ya maji katika vijiji 43 imekamilika na miradi mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Mkoa wa Ruvuma umetengewa jumla ya shilingi bilioni 13.17 kwa ajili ya miradi ya maji vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea na mipango ya kuboresha huduma ya maji katika Miji ya Songea, Mbinga, Namtumbo na Tunduru ya Mkoa wa Ruvuma. Kwa Mji wa Songea, Serikali imekamilisha mradi wa ukarabati wa chanzo cha maji cha Mto Ruhila Darajani kwa gharama ya shilingi bilioni 2.6 ambapo umeongeza kiasi cha maji lita milioni sita kwa siku. Mradi huo umekamilika mwezi Februari, 2016 na sasa upo kwenye majaribio. Kukamilika kwa mradi huo kumewanufaisha wakazi 164,162 wa Manispaa ya Songea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango wa muda mrefu Serikali imekamilisha usanifu wa kina na uandaaji makabrasha ya zabuni kwa ajili ya uboreshaji huduma ya maji katika Miji ya Tunduru, Namtumbo na Mbinga. Utekelezaji wa miradi hiyo utagharimu Dola za Marekani milioni 7.3 kwa Mji wa Tunduru, Dola milioni 12.08 kwa Mji wa Namtumbo na Dola milioni 11.86 kwa Mji wa Mbinga.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-
Wananchi wengi katika Jimbo la Kyerwa wanakabiliwa na tatizo kubwa la upatikanaji wa maji safi na salama, jambo linalorudisha nyuma shughuli za maendeleo:-
Je, ni lini Serikali itatumia maji ya Mto Kagera kuwapatia wananchi maji safi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa muda mfupi, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 200 kwa mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji katika Miji ya Rubwera na Rwenkorongo ambayo ni Makao Makuu ya Wilaya ya Kyerwa. Kazi zilizopangwa kutekelezwa ni pamoja na ununuzi wa mabomba, uchimbaji wa mitaro na ulazaji wa bomba za kusambaza maji pamoja na viungo vyake; kukarabati tanki moja na ununuzi wa pampu mbili za kuvuta na kusukuma maji toka kwenye visima virefu viwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa muda mrefu, kupitia Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imepanga kukamilisha mradi mkubwa wa maji kwa ajili ya Mji wa Kyerwa pamoja na vijiji vinavyozunguka. Taarifa ya upembuzi yakinifu itakapokamilika, ndipo tutawezesha kufanya maamuzi iwapo Mto Kagera ndiyo utumike kama chanzo au kama kuna vyanzo mbadala ambavyo vinaweza kutumika ambapo uzalishaji wa maji utakuwa wa gharama nafuu zaidi na endelevu.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Manispaa ya Kigoma-Ujiji unaogharimu shilingi bilioni 32 ambao unafadhiliwa na Shirika la KFW la Ujerumani na Jumuiya ya Ulaya ulipangwa kukamilika mwezi Machi, 2015:-
(a) Je, kwa nini mradi huo umechelewa kukamilika kwa mujibu wa mkataba?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani dhidi ya Mkandarasi kwa kuchelewa kukamilisha mradi huo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabwe Ruyagwa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa Manispaa ya Kigoma unaogharamiwa na Serikali kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya KFW kwa gharama ya Euro milioni 16.32 sawa na shilingi bilioni 39.13.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa mradi huu unaotekelezwa na Mkandarasi Spencon Services Limited ulianza mwezi Machi, 2013 na ulitarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2015. Hata hivyo, baada tu ya kuanza kwa ujenzi Mkandarasi alichelewa kupewa eneo la ujenzi kutokana na matatizo ya fidia. Hali hii ilisababisha Mkandarasi kupewa nyongeza ya muda wa kazi hadi kufikia mwezi Disemba, mwaka 2015. Pia, kubadilika kwa Menejimenti ya Spencon Services Limited na mtaji mdogo kifedha kumechangia kuchelewa kwa ukamilishaji wa mradi wa maji ambapo hadi kufikia mwezi Oktoba, 2016 utekelezaji wa mradi ulikuwa umefikia wastani wa asilimia 66.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia masharti ya mkataba Serikali imechukua hatua dhidi ya Mkandarasi ikiwa ni pamoja na kumkata fedha (Liquidated Damages) ya Euro 1,632,315.27 sawa na shilingi bilioni 3.9 ambayo ni asilimia 10 ya mkataba kuanzia mwezi Januari, 2016. Vilevile Mkandarasi ameagizwa kuongeza nguvu kazi, vifaa na pia kufanya kazi muda wa ziada zikiwemo siku za mapumziko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, Mkandarasi ameandikiwa barua ya kumfahamisha kuwa Wizara imemweka katika kundi la Non Performing Contractors, (Makandarasi wasioweza kufanya kazi) na Mamlaka zinazohusika za PPRA na CRB zimejulishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, miundombinu ya msingi kama matenki amekwishajenga, pampu zote ameleta, wananchi wa Kigoma Mjini wataanza kupata maji kuanzia mwezi Aprili, 2017.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE Aliuliza:-
Kwa kipindi kirefu wananchi wa Halmashauri ya Chalinze wamekuwa katika sintofahamu juu ya lini mradi wa maji wa Wami - Chalinze utakamilika ili wananchi hao waweze kunywa maji safi kama walivyoahidiwa.
(a) Je, Serikali inaweza kueleza ni lini mradi utakamilika?
(b) Kwa kuwa mradi huu umekuwa unakwenda taratibu sana; je, tatizo lake ni nini?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Benki ya Maendeleo ya Waarabu yaani BADEA, Washirika wa Maendeleo (DPs) kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP) na Mkopo kutoka Serikali ya India kupitia Exim Bank kwa pamoja zimetoa jumla ya shilingi bilioni 164 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji Chalinze kwa Awamu ya I, II na III. Gharama
ya utekelezaji wa miradi hiyo ni shilingi bilioni 23.4 kwa Awamu ya I, Awamu ya II ni shilingi bilioni 53.7 na shilingi bilioni 86.9 kwa awamu ya III.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa Awamu ya I na ya II ya mradi wa Chalinze jumla ya vijiji 88 vimenufaika na kupelekea hali ya upatikanaji wa maji Chalinze kufikia asilimia 88 ya wakazi wote waishio katika eneo lote linalopitiwa na mtandao wa maji. Vijiji 12 vya Mwidu, Visakazi, Lulenge, Tukamisasa, Kinonko, Bwawani, Sinyaulime, Gwata, Ngerengere, Kidugalo, Kambi ya Kinonko na Sangasanga ambavyo vipo katika Awamu ya II vitaanza kunufaika na huduma ya maji ifikapo mwishoni mwa mwezi Aprili, 2017 baada ya kukamilika majaribio ya bomba kuu. Vijiji vitatu vya Kwang’andu, Kifuleta na Kwaruhombo vitaanza kupata maji baada ya mkandarasi kufanya maboresho ya pampu
ambazo zimeonekana hazifanyi kazi ilivyotarajiwa. Mkandarasi ameagizwa kuhakikisha pampu hizo zinafanya kazi kabla Juni, 2017.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali inatekeleza mradi katika Awamu ya III ambapo kazi zitakazofanyika ni pamoja na upanuzi wa mtambo wa kuzalisha maji, ujenzi wa mabomba makuu ya kusafirisha maji (kilometa 115), ujenzi wa mfumo wa mabomba yakusambaza
maji (kilometa 1022), ujenzi wa matanki makubwa 19 na ujenzi wa vituo tisa vya kuchotea maji na ujenzi wa vioski vya kuchotea maji 351. Awamu hii kimkataba ilitakiwa iwe imekamilika tarehe 22 Februari, 2017, mpaka sasa ni asilimia 23 tu ya kazi ndiyo imefikiwa. Serikali imechukua hatua za kimkataba ikiwemo kutoa notice ya siku 100 ili aongeze kasi vinginevyo tutasitisha mkatabaifikapo tarehe 31 Mei, 2017.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA Aliuliza:-
Serikali imeweka pesa nyingi sana katika mradi wa umwagiliaji uliopo katika Kijiji cha Ikweha, Kata ya Ikweha, lakini unashindwa kuanza kwa kuwa Serikali imeshindwa kujenga bwawa.
(a) Je, ni lini mradi huu utakamilika ili kutoa ajira kwa vijana walio wengi katika Kijiji cha Ikweha?
(b) Je, Serikali itawachukulia hatua gani wakandarasi waliojenga mradi huu chini ya kiwango?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuendeleza Skimu ya Umwagiaji ya Ikweha, Serikali ilitekeleza mradi huo kwa awamu mbili. Awamu ya kwanza ilitekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 435.9 na awamu ya pili ilitekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 370.7. Baada ya kukamilika kwa awamu hizo kulikuwa na mapungufu mbalimbali ambayo yalibainika na yalitakiwa kurekebishwa ndani ya kipindi cha matazamio ya miezi 12 kilichotarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2016. Hata hivyo, kutokana na ucheleweshaji wa malipo kwa kazi alizokuwa amezifanya iliababisha
ucheleweshaji wa marekebisho wa mapungufu hayo. Kwa sasa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na mkandarasi wamekubaliana marekebisho hayo yaanze kufanyika mwezi Aprili, 2017.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, endapo mkandarasi atashindwa kukamilisha marekebisho hayo yaliyo kwa muda wa matazamio wa miezi 12, Serikali itamchukulia hatua za kisheria kulingana na mkataba ili kumtoza tozo na kutolipa kazi ambazo ziko chini ya kiwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kujenga mabwawa kama hatua muhimu ya kukabiliana na changmoto za mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha usalama wa chakula kupitia kilimo cha umwagiliaji. Serikali katika Bajeti ya mwaka 2017/2018 itafanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa mabwawa mbalimbali ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji likiwemo hili la Ikweha.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Mwaka 2014/2015 Serikali iliahidi kuongeza usambazaji maji katika vijiji 100 vilivyoko umbali wa kilometa 12 kutoka bomba kuu la Ziwa Victoria hadi Kahama na Shinyanga. Serikali ilitenga na Bunge kupitisha shilingi bilioni nne ili kutekeleza mradi huo.
(a) Je, ni vijiji vingapi vimeshapatiwa maji kati ya hivyo vijiji 100 hadi sasa?
(b) Je, Serikali inafikisha lini maji ya Ziwa Victoria katika vijiji vya Mwakuzuka, Mwaningi, Kabondo, Ntundu, Busangi, Buchambaga, Nyamigege, Gula, Izuga, Buluma, Matinje na Bubungu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kuunganisha vijiji vilivyopo umbali wa kilometa 12 kutoka bomba kuu la Ziwa Victoria hadi Kahama na Shinyanga unatekelezwa chini ya programu ya maendeleo ya sekta ya maji. Katika awamu ya kwanza ya utekelezaji vijiji 40 viliainishwa, kati ya hivyo vijiji 32 vimefanyiwa usanifu. Hadi sasa jumla ya vijiji 13 uunganishaji umekamilika na vijiji hivyo ni Nyashimbi, Magobeko, Kakulu na Butegwa, hilo ni Jimbo la Msalala. Ng’homango, Kadoto, Jimondoli, Mwajiji, Ichongo, Lyabusalu na Bukamba hili ni Jimbo la Shinyanga Mjini na Runere na Gatuli hii ni Kwimba; na vijiji viwili vilivyopo Shinyanga Vijijini ambavyo ni Mwakatola na Mwasekagi uunganishaji unaendelea. Hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 1.96 zimetumika kwa ajili ya kuunganisha maji kwa vijiji hivyo kutoka bomba kuu la Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vya Mwakuzuka, Kabondo, Ntundu, Busangi, Nyamigenge na Gula vipo katika mpango wa awamu ya kwanza na usanifu wake umekamilika na ujenzi unatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2017/2018. Aidha, Serikali itaendelea kuunganisha vijiji vilivyobaki vikiwemo vijiji vya Mwaningi, Buchamba, Izuga, Buluma, Matinje na Bubungu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA aliuliza:-
Serikali imeahidi kujenga mabwawa ya maji katika Kata za Kanoni, Igarwa, Ihanda na Chenyoyo ili kuwapatia wananchi wa kata hizo maji.
(a) Je, Serikali imefikia hatua gani katika kutekeleza kazi hiyo?
(b) Je, Serikali inawahakikishiaje wananchi wa vijiji vya Kafunjo, Kijumbura na Bweranyange kwamba mradi wa maji wa Lyakajunju utakapotekelezwa utawaachia wananchi miundombinu ya maji ili kuwanusuru kuliwa na mamba wanapofuata maji ziwani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa, Mbunge wa Jimbo la Karagwe, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza ujenzi wa mabwawa, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeziagiza Halmashauri zote nchini kuainisha maeneo yanayoweza kujengwa mabwawa na kutenga fedha kwenye bajeti zao za kujenga angalau bwawa moja kila mwaka. Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe imeweza kuainisha maeneo yanayofaa kujengwa mabwawa kama ifuatavyo:-
Kata ya Kanoni eneo la Kabare na Omukigongo, Kata ya Igurwa eneo la Omukalinzi (Kabulala A) na Kata ya Nyakahanga eneo la Kashanda (Karazi). Mabwawa katika maeneo hayo yatajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha baada ya kazi za usanifu, kuandaa michoro, kuainisha gharama na nyaraka za zabuni kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ipo katika hatua za usanifu wa kina wa utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Bwawa la Lwakajunju ambao kutekelezwa kwake kutavipatia huduma ya maji vijiji vyote vitakavyopitiwa na bomba kuu la maji katika umbali usiozidi kilometa 12 kutoka eneo la bomba kuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya usanifu kukamilika itaainisha iwapo vijiji vya Kafunjo, Kijumbura na Bweranyange vitakuwa ndani ya kilometa 12 kutoka eneo la Bomba Kuu. Mradi huo utavipatia maji na endapo havitakuwepo basi Halmashauri iweke kwenye vipaumbele vijiji hivyo katika bajeti inayotengwa na Wizara kila mwaka.
MHE. MARY P. CHATANDA (K.n. y. MHE. STEPHEN H. NGONYANI) aliuliza:-
Serikali ilitenga shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Mkomazi lakini baadaye Serikali ilihamishia fedha hizo Mkoa mwingine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha pesa hiyo ili Bwawa lililokusudiwa lijengwe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stephen Hillary Ngonyani, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 2003 na 2004 wananchi wa kijiji cha Manga Mkocheni, kata ya Mkomazi, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe walionesha hitaji la mradi wa kuendeleza kilimo cha umwagiliaji kwa zao la mpunga katika Bonde la Mkomazi. Aidha, mwaka wa fedha 2006/2007 Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa wakati huo kupitia Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Kilimanjaro ilifanyika upembuzi yakinifu na usanifu wa awali ambapo walibaini kuwa jumla ya shilingi bilioni kumi na tatu zingehitajika kuendeleza Bonde la Mkomazi ikiwemo ujenzi wa bwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Hata hivyo, usanifu huo ulibaini kuwa bwawa hilo lingezamisha Ziwa Manga lililopo katika Kijiji cha Manga, ambalo lina maji ya chumvi ambayo yangeathiri kilimo cha zao la mpunga. Kutokana na changamoto hii mwaka wa fedha 2014/2015 Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Kilimanjaro ilianza kufanya mapitio ya upembuzi yakinifu na usanifu kwa kuepuka kuzamisha Ziwa Manga na kubaini kuwa jumla ya shilingi bilioni 1.5 zingehitajika kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufikia azma hii Serikali kupitia bajeti ya mwaka 2015/2016 ilitenga jumla ya shilingi milioni mia nane kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Mkomazi. Hata hivyo bajeti ya maendeleo kwa fedha za ndani iliyotengwa kwa ajili ya miradi ya umwagiliaji ikiwemo Bwawa la Mkomazi haikutolewa na hivyo kusababisha mradi huo kutotekelezwa. Sambamba na fedha hizo kutotolewa bado kuna baadhi ya wananchi ambao walikuwa wanaukataa mradi kwa sababu ya maeneo yao kuzamishwa ndani ya maji na hivyo kufanya mazingira ya kutekeleza mradi huo kutokuwa rafiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi walio wengi wa Kata ya Mkomazi kupitia Mheshimiwa Mbunge bado wanaona umuhimu wa mradi huo na hasa katika hatua za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, Wizara yangu kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji italiingiza bwawa hili katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanza utekelezaji ili hatimaye lengo la Serikali na wananchi wa Mkomazi waweze kuwa na kilimo cha uhakika na hivyo kuwa na usalama wa chakula na kujiongezea kipato kupitia zao la mpunga.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA (K.n.y. PHILIPO A. MULUGO) aliuliza:-
Mji wa Mkwajuni ndio Makao Makuu ya Wilaya mpya ya Songwe. Katika mji huu hakuna maji na idadi ya wananchi na wakazi wanaongezeka kwa kasi:-
Je, ni lini Serikali itajenga miradi katika mji huu pamoja na sehemu nyingine zisizo na maji katika Jimbo la Songwe?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Philipo Augustino Mulugo, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la upungufu wa maji katika Mji wa Mkwajuni lililosababishwa na ongezeko la watu mara baada ya kutangazwa kwa Mji wa Mkwajuni kuwa Makao Makuu ya Wilaya ya Songwe.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuweza kutatua changamoto za upatikanaji wa maji safi na salama katika Jimbo la Songwe. Katika kuboresha huduma ya maji katika Halmashauri ya Songwe, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 694.7 kwenye Bajeti ya Mwaka 2017/2018 ili kuhakikisha hali ya upatikanaji wa maji inaendelea kuimarika.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 katika Bajeti ya Mwaka 2017/2018 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa vitabu vya zabuni katika Mji wa Mkwajuni ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Songwe. Kukamilika kwa kazi hiyo kutatoa gharama halisi ya utekelezaji wa mradi mkubwa katika Mji wa Mkwajuni.
MHE. JASSON S. RWEIKIZA aliuliza:-
Kuna mradi mkubwa wa maji wa siku nyingi pale Maruku (Kyolelo) ambao miundombinu yake mikubwa kama matanki, mabomba chini ya ardhi na vyanzo vyake ni vizuri lakini kutokana na uchakavu mradi huo hautoi maji; mradi huo ulikuwa ukihudumia vijiji vitano katika Kata za Kanyangeneko na Maruku; kukarabati miundombinu iliyochakaa inaweza kugharimu kiasi kidogo cha fedha kama shilingi milioni 500 kwa kuhudumia vijiji vitano wakati mradi mmoja kwa kijiji kimoja wa miradi inayoendelea unagharimu zaidi ya shilingi milioni 800.
Je, Serikali haioni ni busara kuukarabati mradi huu haraka?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mradi wa Maji wa Maruku- Kanyangereko ni miongoni mwa miradi iliyoanza kujengwa baada ya Tanzania Bara kupata Uhuru mwaka 1961. Mradi ulijengwa na ulikamilika mwaka 1977 na kuanza kutoa huduma. Mradi huu ulikuwa ukiendeshwa na Serikali chini ya usimamizi wa Idara ya Maji ngazi ya Mkoa. Hadi kufikia mwaka 1983, mradi ulikuwa unafanya kazi lakini ulisimama kwasababu ya wananchi kutochangia fedha za uendeshaji na matengenezo ikiwa ni pamoja na kuhujumiwa kwa miundomibu ya mradi. Aidha, wananchi hawakupewa elimu ya kutosha ya kutambua kuwa mradi huo ni wa kwao na wanatakiwa kuutunza.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri imewasilisha maombi Wizarani ya kukarabati mradi huu kupitia miradi ya maji iliyoko kando kando ya Ziwa Victoria itakayofadhiliwa na Serikali ya Japan kupitia Shirika la maendeleo ya JICA.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba imepanga kutekeleza mradi huu kupitia Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP II) na inatarajiwa kuwa mradi huu utaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2017/2018 ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.278 kimetengwa kwa ajili ya Halmashauri ya Bukoba. Ukarabati wa mradi huo utatekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza:-
Kuna miundombinu ya kusambaza maji safi na salama iliyokamilika lakini inatoa huduma chini ya kiwango cha ujenzi wake (below design and built capacity).
(a) Je, ni miradi mingapi ya maji safi na salama inayotoa huduma chini ya uwezo wa usanifu na ujenzi wake kutokana na vyanzo kupungua au kukauka maji?
(b) Je, ni hatua zipi zinachukuliwa kuepusha miradi mingine kukumbwa na matatizo kama hayo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, miradi iliyosanifiwa na kujengwa inaweza kutoa huduma ya maji chini ya kiwango kutokana an sababu mbalimbali ikiwemo uchakavu wa miundombinu iliyojengwa, ongezeko la matumizi, uharibifu wa miundombinu, kupungua au kukauka kwa vyanzo vya maji kunakoweza kusababishwa na uharibifu wa vyanzo vya maji kutokana na shughuli za kibinadamu na mabadiliko ya tabia nchi. Kwa takwimu hivi sasa jumla ya miradi 114 nchini kote imebainika kutoa huduma ya maji chini ya kiwango tofauti na ilivyosanifiwa.
Mheshimiwa Spika, ili kuepusha miradi mingine kukumbwa na matatizo kama hayo, Wizara imeandaa na inatekeleza mkakati wa kutunza na kuhifadhi vyanzo vya maji wa mwaka 2014 na mpango wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi wa mwaka 2013 ili kuhakikisha vyanzo vya maji vinakuwa endelevu.
Mpango huo unatekelezwa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kwa kutoa elimu kwa wananchi ambao wananchi wanahamasishwa kutokufanya shughuli za kibinadamu katika umbali usiopungua mita 60 kutoka kwenye mito na vijito na mita 500 kutoka kwenye bwawa na kuondoa watu wote wanaofanya shughuli za kibinadamu katika maeneo ya vyanzo vya maji na maeneo oevu kwa maeneo hayo kupandwa miti rafiki kwa ajili ya kurejesha uoto wa asili.
MHE. LEONIDAS T. GAMA aliuliza:-
Wananchi wangu wa Jimbo la Songea Mjini katika eneo la Matogoro, Mahiro, Lihira na Chemchem walitoa maeneo ya kilimo na makazi kwa SOUWASA ili kutengeneza bwawa la maji kwa Mji wa Songea toka mwaka 2003 na jumla ya wananchi 872 walifanyiwa uthamini wa mali na nyumba zao. Mwaka 2015 uthamini ulifanyiwa marejeo (review) na jumla ya kiasi cha shilingi 1,466,957,000 iliidhinishwa na Serikali kama madai halali ya wananchi hao lakini hadi leo ni miaka 14 imepita wananchi hao hawajapewa stahili zao.
(a) Je, Serikali haioni kuwa kitendo hiki cha kutowalipa wananchi haki zao ni kuwaongezea umaskini wa kipato, malazi na kukosa uwezo wa huduma za matibabu na elimu?
(b) Je, ni lini Serikali itawalipa wananchi hao stahiki yao waliyotakiwa kulipwa miaka mingi iliyopita?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leonidas Tutubert Gama, Mbunge wa Songea Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mwaka 2006 Serikali ililipa kiasi cha shilingi 20,695,051 kwa wananchi 64 kwa ajili ya fidia ya Wananchi waliopisha ujenzi wa miundombinu ya Bwawa la Ruhila. Wananchi hao ni wale ambao walikuwa nje ya mita
60. Wananchi 872 ambao walikuwa ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo cha Mto Ruhila walifanyiwa tathmini mwaka 2003. Kwa mujibu wa Sheria ya mazingira ya mwaka huo wa 2004 wananchi hao hawastahili kulipwa fidia.
Mheshimiwa Spika, wananchi hao walitoa malalamiko yao kwa Serikali ambapo Serikali imepitia Sheria ya mazingira ya mwaka 2004 na kuona kwamba ilitungwa wakati Wananchi wameshafanyiwa tathmini. Aidha, tathmini hiyo ilipitiwa upya mwaka 2015 na kubaini jumla ya shilingi 1,466,957,000 zinahitajika kulipwa fidia. Serikali imepanga kulipa fedha hizi fidia katika mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. HAWA M. CHAKOMA (K.n.y. MHE. ALLY S. UNGANDO) aliuliza:-
Wananchi wa Mji wa Kibiti wamefanikiwa kupata mradi wa maji, ingawa una changamoto nyingi katika utendaji wake:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku kwa ajili ya kulipia umeme na kulipa vibarua?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza usambazaji maji na mtandao, hasa ikizingatiwa kuwa, Mji huo unaendelea kukua kwa kasi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimia Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti, lenye Sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inafahamu juu ya gharama zinazohusika katika uendeshaji wa Mamlaka za Maji kuwa ni pamoja na kulipa umeme na wafanyakazi wanaohusika katika uendeshaji huo. Kwa mujibu wa Sheria Namba 12 ya Huduma ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira ya Mwaka 2009, Halmashauri za Wilaya zimepewa wajibu wa kusimamia uendeshaji wa mamlaka katika kutoa huduma ya maji safi kwa wananchi katika miji yao, hivyo ni matarajio ya Serikali kuwa, Halmashauri ya Mji wa Kibiti inatimiza wajibu wake huo kwa kuwezesha ugharamiaji kwa kupitia bajeti zake na makusanyo kutokana na matumizi ya maji katika Mji wa Kibiti.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inafahamu ongezeko kubwa la watu linalosababisha kupanuka pia kwa eneo la Mji wa Kibiti. Kwa ufahamu huo katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, jumla ya Sh.568,477,000/= zimetengwa kwa ajili ya kuboresha huduma ya mji safi na usafi wa mazingira katika Halmashauri ya Mji wa Kibiti. Fedha hizo zitatumika katika kuongeza mtandao wa mabomba wenye umbali wa kilometa tano pamoja na kufufua visima vilivyopo ili kuongeza uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Mji wa Kibiti, itaendelea na uwezeshaji katika ujenzi wa miradi ya maji kwa lengo la kuongeza na kuboresha zaidi upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Mji wa Kibiti na Tanzania kwa ujumla.
MHE. DKT. HAJI H. MPONDA aliuliza:-
Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo (SAGCOT) imekamilisha ujenzi wa Skimu ya Umwagiliaji, Itete ambapo imehusisha ujenzi wa miundombinu ya banio na mfereji mkuu wa kilometa 6.6, lakini katika kipindi kifupi cha matumizi ya skimu hii mfereji huo mkubwa umeshaanza kuharibika kutokana na kiwango duni cha ujenzi:-
(a) Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa mfereji mkuu na mifereji ya kati, ili kuendeleza kilimo katika hekta 7,000 zilizobaki katika skimu hiyo?
(b) Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa mfereji mkuu uliobomoka katika kipindi hiki cha uangalizi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Jimbo la Malinyi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa mradi wa umwagiliaji katika Skimu ya Itete ulianza mwezi Mei, 2013 na kukamilika mwezi Oktoba, 2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, upanuzi wa mradi huu unategemea kwa kiwango kikubwa kiasi cha maji katika Mto Mchilipa, kwani usanifu wa awali ulibainisha hekta 1,000 ambazo ndizo zilizoendelezwa. Ili kuweza kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji katika eneo lililobaki Serikali inajipanga kufanya upembuzi yakinifu kuona kama kuna uwezekano wa kujenga bwawa ili kutunza maji ya mvua ya Mto Mchilipa, ambayo yatatumika katika kuendeleza eneo lililobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ndogo iliyobomoka ya mfereji, Wizara yangu kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Kanda ya Morogoro imeshafanya mawasiliano na Mkandarasi aliyejenga skimu hiyo na amekubali kufanya marekebisho katika sehemu hiyo katika kipindi cha uangalizi.
MHE. ALEX R. GASHAZA (K.n.y. MHE. OLIVER D.
SEMUGURUKA) aliuliza:-
Katika Halmashauri ya Wilaya ya Ngara kuna matatizo makubwa sana ya maji kiasi kwamba wananchi wa maeneo hayo wanaona kuwa kupata maji ya bomba ni kama ndoto isiyowezekana na wamekuwa wakilipishwa gharama ya maji hata kwa wateja ambao hawapati kabisa huduma ya maji kwa kipindi cha mwezi husika ikiambatana na shilingi 1,500 kila mwezi kwa ajili ya mita ya maji.
(a) Je, Serikali inakubaliana na tozo ya shilingi 1,500 ya lazima kwa malipo ya mita?
(b) Je, Serikali inawaambia nini wananchi wanaotozwa bili za maji wakiwa hawajapata huduma ya maji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika uendeshaji wa mamlaka na utoaji bora wa huduma ya maji, tozo ya shilingi 1,500 ilipitishwa na EWURA mwaka 2011 kwa mchanganuo ufuatao:-
(i) Shilingi 500 service charge; na
(ii) Shilingi 1,000 meter rent.
Mheshimiwa Naibu Spika, tozo hii iliendana na bei ya maji inayotumika hadi sasa. Kutokana na tarrifs mpya za EWURA ambazo zimeondoa tozo hiyo kwa sasa Mamlaka ya Maji Mjini Ngara inaandaa andiko la mpango wa biashara (business plan) litakalowasilishwa EWURA kwa ajili ya mapitio ya bili hiyo na kupata bili mpya ya maji inayoendana na wakati uliopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na malalamiko yaliyopo kuhusu baadhi ya wananchi kupelekewa ankara wakati hawapati huduma ya maji, Wizara itafuatilia kwa kina kujua kama ni kweli tatizo hilo lipo na endapo itabainika hatua stahiki zitachukuliwa.
MHE. DKT. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-
Katika Jimbo la Masasi, Kata za Marika, Mumbaka, Matawale, Sululu, Mwenge, Mtapika, Temeke na Chanikanguo, kuna tatizo kubwa la maji wakati eneo la katikati ya mji linanufaika na maji ya mradi wa Mbwinji.
Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kutosha kwa ajili ya upanuzi wa mradi wa maji wa Mbwinji ili usambaze maji katika vijiji vya Jimbo la Masasi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Jimbo la Masasi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Safi wa Masasi, Nachingwea kutoka chanzo cha Mbwinji unahudumia wakazi wa Miji ya Masasi na Nachingwea pamoja na baadhi ya vijiji vya Halmashauri za Wilaya ya Masasi Nachingwea na Ruangwa. Jumla ya wakazi wapatao 188,250 wanahudumiwa na mradi huo uliojengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 31 na kuzinduliwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete tarehe 24 Julai, 2014.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali imeendelea kuunganisha vijiji zaidi ili kuongeza upatikanaji wa maji kupitia mradi huo. Kwa sasa baadhi ya vijiji katika Kata za Marika, Mumbaka, Matawale, Sululu, Mwenge, Mtapika, Temeke na Chanikanguo, vimeanza kupata maji na vijiji vilivyobaki katika Kata hizo vitaendelea kuunganishwa kutoka kwenye mradi huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika bajeti ya mwaka 2016/2017 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuendelea kuunganisha vijiji vilivyobaki na katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Serikali imetenga shilingi bilioni moja ambapo hadi sasa shilingi milioni 370 zimeshatolewa kwa ajili ya kuendelea kuunganisha vijiji vilivyobaki kwenye Mradi wa Masasi, Nachingwea.
Mwasa MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-
Kwa kuwa bwawa linalotarajiwa kuchimbwa katika Kijiji cha Mbwasa, Tarafa ya Kintinku ni bwawa la kimkakati kwa wakazi wa Tarafa nzima ya Kintinku.
Je, ni lini Serikali itaanza rasmi ujenzi wa bwawa hilo baada ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kukamilika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni ilipanga kujenga Bwawa la Mbwasa kwa kupitia Mto wa Msimu wa Luwila ikiwa ni hitaji la wananchi wa Kijiji cha Mbwasa kwa ajili ya shughuli za kilimo, mifugo na matumizi ya nyumbani. Ujenzi wa Bwawa la Mbwasa ulikusudiwa kunufaisha pia wananchi wa vijiji vya jirani vya Mwiboo, Mtiwe na Chikuyu, lengo kuu ikiwa ni kuimarisha kilimo cha umwagiliaji wa zao la mpunga. Hali hii inatokana na maeneo hayo kutokuwa na uhakika wa mvua za kutosha kwa ajili ya uzalishaji wa mazao ya kilimo.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013, upembuzi yakinifu na usanifu wa Bwawa la Mbwasa ulifanyika kupitia Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Dodoma. Aidha, matokeo ya upembuzi huo yalibaini kuwa jumla ya shilingi 2,500,000,000 zingehitajika kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hilo. Hata hivyo, bajeti za maendeleo za fedha za ndani iliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ya umwagiliaji ikiwemo Bwawa la Mbwasa haikutolewa na hivyo kusababisha ujenzi wa bwawa hili kutotekelezwa.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara yangu kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ilianza kufanya mapitio ya Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa Mwaka 2002. Kwa kutambua umuhimu wa ujenzi wa mabwawa kama hatua ya kimkakati ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Bwawa la Mbwasa limepewa kipaumbele na litaingizwa katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanza utekelezaji ili hatimaye lengo la Serikali na wananchi wa Kijiji cha Mbwasa pamoja na vijiji vya jirani kuwa na kilimo cha uhakika.
MASHIMBA M. NDAKI aliuliza:-
Serikali imekamilisha mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria hadi Mji wa Ngudu na vijiji vilivyo karibu na mji huo Wilayani Kwimba. Mradi huo unatoa maji ya uhakika kuliko miradi ya visima vifupi ambavyo ni vya msimu. Lakini Mji Mdogo wa Malampaka na vijiji vingine vya karibu kama Jihu, Bukigi, Muhida, Lali, Nyabubinza na Mwang’honoli ambavyo vipo karibu na Mji wa Ngudu havijaunganishwa kwenye mradi huo.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuunganisha Mji Mdogo wa Malampaka na vijiji vya Jihu, Bukigi, Muhida, Lali, Nyabubinza na Mwang’honoli katika mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria ili kuwapatia wananchi maji ya uhakika?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mradi wa maji safi toka Ziwa Victoria kwenda katika Mji wa Ngudu na vijiji vilivyopo kandokando ya bomba linalopeleka maji katika mji huo. Vijiji hivyo ni Runele, Ngatuli, Nyang’onge, Damhi na Chibuji. Mradi huu ulihusu ulazaji wa bomba kilometa 25 na sehemu nyingine ya bomba lilitumika bomba la zamani la mradi wa visima uliojengwa miaka ya 1970. Bomba hilo ni la kipenyo cha inchi nane na kulingana na usanifu halitoshi kuendeleza zaidi kwenda Malampaka.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji…

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji imetekeleza Miradi ya Maji ya Malampaka, Sayusayu, Masayi, Njiapanda na Sangamwalugesha ambayo imekamilika na wananchi wanapata maji. Miradi ya Maji ya Lalago, Mandang’ombe na Jija inaendelea kujengwa na ujenzi umekamilika kwa asilimia 65. Serikali pia imekamilisha usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni kwa Miradi ya Maji ya Mwabulimbu, Mwamanenge na Badi ambao utahudumia vijiji vitatu vya Muhiba, Jihu na Badi yenyewe. Ujenzi wa miradi hii utafanyika katika Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza miradi hii kwa awamu, hivyo, kwa vijiji ambavyo havipo katika awamu hii tunaomba Mheshimiwa Mbunge awasiliane na halmashauri husika ili viwe katika kipaumbele katika awamu zinazokuja.
MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Wilaya ya Kaliua inakabiliwa na tatizo kubwa sana la maji hali inayosababisha wananchi wake wengi kuteseka kwa kukosa huduma hiyo muhimu na kutumia muda mwingi kutafuta maji umbali mrefu na hivyo kushindwa kufanya shughuli za maendeleo.
Je, mradi mkubwa wa kutoka Mto Malagarasi kwenda vijiji vya Kaliua mpaka Urambo utaanza lini na kukamilika lini?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua tatizo la maji katika vijiji vya Kaliua hadi Urambo, Serikali imeanza kutekeleza mradi wa kutoa maji Mto Malagarasi kwa kumuajiri mtaalam mshauri ambaye anaendelea na kazi ya usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni ya ujenzi. Kazi hiyo imepangwa kukamilika mwezi Oktoba, 2017.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mbili kwa ajili ya usanifu wa mradi huo. Aidha, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, na mara fedha zitakapopatikana, itajulikana ujenzi wa mradi huo utaanza lini na kukamilika lini.