Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kunti Yusuph Majala (31 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii nami katika Bunge hili niweze kuchangia Wizara inayoamua Watanzania leo tuendelee kuishi ama la. Wizara ya Afya ni Wizara nyeti sana, ndiyo inayosababisha sisi leo tuko humu ndani tukiwa na afya njema pamoja na Mwenyezi Mungu kutujalia. Wizara hii ni Wizara ambayo bado inachechemea. Wizara ambayo inakwenda kuamua hatima ya maisha ya Mtanzania, bado tunakwenda kuiletea mzaha na kufanya ushabiki kwenye maisha ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni takribani miaka 55 ya uhuru, hatuna Vituo vya Afya ndani ya Kata zetu 3,990. Tuna vituo vya afya ambavyo havifiki 500, halafu tuko humu ndani leo tunajisifu, tunapongezana kwa makofi eti kana kwamba tunakwenda kufaulu. Hatufaulu, tunarudi nyuma na tunaendelea kutokuwatendea haki Watanzania. Hali ya hospitali zetu kwenye maeneo yetu tunakotoka; tuachane na hospitali hizi za mjini, hebu twende kule vijijini. Mheshimiwa Waziri hotuba yake nikiiangalia na kuisoma imelenga maeneo ambayo yako hapa mbele yetu. Haijatugusa kule vijijini!
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijijini hospitali zetu zinasikitisha, zinatia huruma, wananchi wetu wanapata tabu. Hospitali zisizokuwa na maji! Hospitali zisizokuwa na umeme. Mbali na maji na umeme, lakini hospitali hizi hazina Wauguzi, hazina Madaktari, hazina madawa! Tunawatakia nini hawa Watanzania? Shida yetu ni nini? Si mtwambie Chama cha Mapinduzi miaka 55 mmeshindwa kuleta hoja ya msingi ya kuweza kuokoa maisha ya Watanzania! Tunabaki tunapigiana makofi humu ndani! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuachane tu na suala zima la hali mbovu za hospitali, uwepo wa hizo hospitali zenyewe! Mkoa wangu wa Dodoma wenye Wilaya saba, tuna Wilaya nne tu ndiyo zina hospitali; Wilaya tatu hizi hazina Hospitali za Wilaya. Mnaweza mkasema Wilaya ya Chemba ni mpya, Wilaya ya Bahi ni mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chamwino ambayo awali ilikuwa inaitwa Wilaya ya Dodoma Vijijini mpaka leo ambako Ikulu ipo ya Chama cha Mapinduzi, hawana hospitali wale wananchi! Wanatoka Vijiji vya Chamwino, Mtera huko imepakana na Iringa wanasafiri kuja Manispaa ya Dodoma kupata huduma. Hivi mnawatakia wema kweli hawa Watanzania wa Mkoa wa Dodoma? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambieni tu ndugu zangu, katika mikoa ambayo inawakoa, bado inasuasua ni Mkoa wa Dodoma ndiyo ambao angalau mnaambulia, lakini Waswahili wanasema usimwamshe aliyelala, utalala mwenyewe. Ipo siku wananchi hawa watakuja kuchoka na mateso na ahadi kila kunapokucha, mnaenda kuwaahidi kwamba tutawaleteeni hospitali ambazo hamzipeleki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma zinazotolewa kwenye hospitali zetu, wenzangu wamesema, naomba niongezee. Niende huduma zinazotolewa kwenye huduma ya mama mjamzito. Huduma zinazotolewa kwenye hospitali zetu kwa mama mjamzito, zinawakatisha tamaa wanawake kwenda hospitalini ndiyo maana wengine wanaamua kuzalia majumbani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wa kike ambao hawajafikisha umri wa miaka 18 kwa Dini ya Kiislamu mtoto anaweza kuolewa hata miaka 14, 15, 16; mtoto huyu akiolewa akipata ujauzito akienda hospitalini kwa ajili ya kujifungua, hapewi huduma. Atapewa kashfa kibao, atapewa matusi ya kila aina na kumsababishia mtoto yule hata kukosa ujasiri wa kwenda kutimiza wajibu na jukumu lake katika Taifa lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lugha hizi zinatusababishia vifo vingi vinavyokwenda kuwapoteza akinamama, vinavyokwenda kuwapoteza watoto ambao tunahitaji kesho na wao waje watupokee mzigo huu tulionao katika Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wanawake ambao wana umri mkubwa kuanzia miaka 40, hawa nao imekuwa ni changamoto kwenye hospitali zetu. Wakifika Hospitalini, “limama jitu zima, limebebelea limimba mpaka leo linazaa! Hizo ni lugha ambazo zinatolewa na wafanyakazi wetu kwenye hospitali zetu. Mheshimiwa Waziri wewe ni mwanamke, unajua uchungu wa kuzaa…
MWENYEKITI: Siyo wote ni baadhi! Ni baadhi, siyo wote!
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni baadhi!
Mheshimiwa Waziri unajua jinsi wanawake tunavyopata tabu, lakini kuna mwanamke mwingine yawezekana kwenye usichana wake amehangaika kupata mtoto ameshindwa. Imefika umri wa miaka 40 huyu mtu kabahatika kupata hiyo mimba, asizae? Kwa nini baadhi ya hawa watumishi wasipewe onyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona wiki iliyopita Mbeya, Muuguzi alichomtendea yule mama aliyekuwa anajifungua pale, Mkuu wa Mkoa alikwenda pale hospitalini. Yule mama anaeleza kwa uchungu namna alivyofanyiwa na mhudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli tunataka kuwatendea haki hawa wanawake? Tunataka kweli wanawake hawa waendelee kuja kwenye hospitali zetu kwa ajili ya kupokea kejeli, matusi na kashfa! Ya kazi gani? Vifo vya wanawake vinasababishwa na hizi kashfa; wanawake wengi wanashindwa kwenda hospitali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake pia tunashindwa kwenda Hospitali kujifungua mahali salama; siyo salama, pale napo tunakwenda kutafuta vifo vingine. Ukienda hospitalini, kaka yangu Mheshimiwa Kuchauka amesema, unaambiwa mwezi wako wa mwisho, mwezi wa Nane unaenda wa Tisa kwenda kujifungua, utaambiwa unapokuja njoo na ndoo; maeneo ambayo hayana maji, anaambiwa aende na maji mama mjamzito. Maeneo ambayo hayana umeme, mama anaambiwa aende na taa au mafuta ya taa ili aweze kupata huduma ya kuweza kutimiza wajibu wake na majukumu katika Taifa letu ya kuongeza Watanzania katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, CHF, janga la Taifa hili. Tunawatwisha Watanzania mzigo juu ya mzigo. Mmeshindwa kupeleka dawa; ili mjifiche kwenye kichaka, mmeamua kuwaundia mradi unaoitwa CHF mwendelee tena kukusanya fedha zao, wakienda hospitalini hakuna dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, CHF hii watu wetu wamekwenda kujiunga; akienda hospitali na kadi ile akifika fursa pekee anayoipata kwenye ile kadi ama huduma pekee ni kwa ajili tu ya kumwona Daktari. Akitoka kwa Daktari, amepata dawa ni paracetamol. Awe anaumwa tumbo atapewa paracetamol, awe amevunjika mguu atapewa paracetamol, awe anaendesha atapewa paracetamol. Ugonjwa wowote huduma pekee atakayoipata ataambiwa paracetamol ndiyo dawa atakayoipata pale, akipata bahati sana ya kupata dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huyu mwananchi anauliza, hivi nimeambiwa na Serikali yangu nijiunge kwenye Mfuko huu ili niweze kuokoa maisha yangu. Hata pale ninapokuwa sina fedha nipate huduma, lakini leo hii wananchi wetu wametoa fedha zao na badala yake wanaenda kuambulia maneno ama kuoneshwa maduka ya kwenda kununua dawa. Mradi huu siyo rafiki kwa Watanzania. Mheshimiwa Waziri tunaomba aje na mbadala wa biashara hii ya CHF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata miradi mingine ya Bima ya Afya, NHIF; ukienda na kadi ile, ukifika pale, kwanza kabla hata hujaitoa, unauliza jamani dirisha la Bima ya Afya liko wapi? Bima ya Afya? Eeh! Mhudumu anaweza akakukata kushoto akaendelea na safari zake. Kama uko kwenye foleni hujauliza chochote, unaulizwa; unatibiwa cash au una Bima? Ukimwambia una Bima, anakwambia subiri, kaa pale! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wenyewe Wabunge imetutokea, mimi nikiwa ni mhanga. Nimeenda Dar es Salaam Agakhan pale. Nimefika nikawaambia naumwa, nina Kadi ya Bima ya Afya – NHIF. Nikaambiwa, dada tunaomba usubiri pale. Nilisubiri zaidi ya dakika 45, nikaona haina sababu ni heri ninyanyuke nijiondokee zangu nikatafute hospitali nyingine nitoe fedha niweze kutibiwa. Sasa sisi kama tuko humu ndani yanakuwa namna hiyo na hizo kadi zenu mlizotupa, walioko kule nje hawa ambao mnawakatia hivi vikadi vyenu inakuwaje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Spika, nami nianze na suala zima la maji. Suala hili limekuwa ni changamoto kubwa sana kwa Watanzania wa nchi hii. Nitazungumzia suala la maji kwa Manispaa ya Dodoma, lakini pia nitazungumzia suala la maji kwa Wilaya ya Chemba.
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Chemba tuna Mradi wa Maji Ntomoko. Mradi huu umeanza mwaka 2014 na ulikuwa una gharama ya shilingi bilioni 2.8. Mradi huu ulitakiwa kuhudumia vijiji 18 lakini ni kwa bahati mbaya sana katika vijiji 18 vijiji nane vikaondolewa vikabaki vijiji 10. Kati
ya hivyo vijiji 10 hivi ninavyoongea hakuna kijiji hata kimoja ambacho kimepata maji kutokana na mradi huo na mpaka sasa mkandarasi ameshalipwa shilingi bilioni 2.4, maji hakuna.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Maji Ntomoko ulidhamiria kupeleka maji kwenye kituo cha afya ambacho kinatumika kama Hospitali ya Wilaya ya Chemba. Hospitali ile haina maji, miundombinu ya maji imeshaharibika. Mwanamke mjamzito anapokwenda hospitalini kupata huduma ya kujifungua sharti ndugu zake waende na ndoo ya maji kichwani ili mwanamke yule aweze kupata huduma ya maji. Kama ndugu zake wakishindwa kwenda na maji mwanamke yule atapata huduma ya kujifungua, atafungashiwa uchafu wake atakwenda nao nyumbani kwake kwenda kupata huduma ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, suala la maji ni kero katika Taifa letu, ni shida katika nchi hii. Tatizo la maji katika Taifa hili siyo suala la upatikanaji wa vyanzo vya maji kwani tunavyo vya kutosha sana. Shida ya Taifa hili ni mfumo wa namna ya kuyasambaza maji hayo kuwafikishia Watanzania kwenye maeneo yao, vyanzo vya maji vipo vya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, maji ya Ntomoko ninayokwambia siyo maji unayokwenda kuyachimba bali ni maporomoko ya maji unakwenda kuyatega wananchi wanapata maji, imekuwa ni shida kweli kweli. Shilingi bilioni mbili watu wamelamba, wamekaa kimya, Watanzania wanapata shida na suala la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mimi niseme ule mradi kwa kuwa ulikuwa ukamilike mwezi wa Pili mwaka huu umeshindikana na hakuna sababu zozote za msingi ambazo Watanzania wa Wilaya ya Chemba wanapewa, tunaomba huo mradi uondolewe kwetu ili tutafutiwe mradi mwingine mbadala utakaoweza kuleta tija na utakaofanya wananchi wetu waweze kupata maji. Nimeamua kulisemea hili kwa Waziri Mkuu ili na yeye aweze kuona kwa jicho la pekee sana hususani kwenye ile hospitali ambayo watu wanakwenda kupata huduma pale. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye suala zima la maafa. Mfuko wa maafa uko kwenye ofisi ya Waziri Mkuu. Kama unavyojua nchi yetu imekumbwa na ukame na hali ya chakula katika Taifa letu siyo nzuri kwenye maeneo kadhaa na hususan katika Mkoa wangu wa Dodoma hali ya chakula ni mbaya sana. Nilisema hapa siku ya Jumatatu kwenye briefing kwamba Watanzania wa Mkoa wa Dodoma
kuna njaa ya kutosha na imekithiri.
Mheshimiwa Spika, hapa ninapoongea, debe la mahindi Dodoma Mjini hapa sokoni pale Mwembeni na Majengo ni Sh.23,000, kilo ya mahindi wanapima Sh.1,250. Kondoa debe ni Sh.25,000, Chemba ni Sh.27,000, Kongwa kwako pale Kibaigwa ni Sh.22,500. Sijaona kwenye kitabu cha Waziri Mkuu akituambia suala la ukame katika Taifa hili katika yale maeneo ambayo yana changamoto ya bei kubwa za mazao ni nini amekifanya au anatarajia kufanya kitu gani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hii si sawa, hatuwatendei haki hawa Watanzania wetu. Watu wanakufa, watu wanajiua, wanaume Wilaya ya Kondoa wawili wameamua kujiua kwa sababu familia zao zimekosa chakula kwa muda wa siku tatu. Wanaume wanakimbia familia zao, wanawake ndiyo
wanaobaki kwenye majumba na watoto wao lakini mwanamke huyo naye mvua Dodoma safari hii haijanyesha ya kutosha. Hata vibarua mwanamke aende akalime apate fedha ya kununua kilo ya mahindi hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ningetaka kujua ni lini Serikali itatuletea chakula watu wa Dodoma. Tunahitaji chakula watu wa Dododma na naamini hata wewe unahitaji chakula kwa ajili ya watu wa Kongwa. Mheshimiwa Waziri Mkuu watu wa Dodoma tunaomba yale mahindi yanayooza Shinyanga tani 8,000 tunazihitaji watu wa Dodoma tuna shida na chakula, acheni kuozesha chakula wakati watu wanakufa kwa njaa. Kama ninyi upande wa pili hamuwezi kusema sisi tuacheni tuseme, tuko hapa kwa ajili ya kuwasemea Watanzania. Hatuko hapa kwa ajili ya kuona nafsi zetu ziko salama lakini kesho tutakuwa huko na sisi mitaani maana yake kazi hii siyo ya kudumu. Niombe nipate ufafanuzi kwenye suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye suala la Mahakama. Mahakama zetu zimekuwa ni changamoto kubwa sana hususani kwenye upande wa watumishi, lakini pia kwenye suala zima la miundombinu kwa maana ya majengo yako. Wilaya yangu ya Chemba haina hata hiyo
Mahakama ya Wilaya tu.
Mheshimiwa Spika, pili, Mahakama hizi za Mwanzo ambazo ziko kwenye Kata zetu kule chini ziko kwenye nyumba za watu ambao wamejitolea, lakini hata hao wahudumu unakuta kuna Karani mmoja na Hakimu mmoja anayeweza kuzunguka kwenye Kata zaidi ya nane, ameenda Kata chache sana ni Kata tano. Tuone ni namna gani tunaongeza Watumishi kwenye sekta hii ama kwenye Wizara hii ya Mahakama ili wananchi wetu waweze kupata huduma hii kwa urahisi lakini pili kwa uharaka ili waweze kuendelea na shughuli zingine. (Makofi).
Mheshimiwa Spika, lingine ni migogoro ya ardhi. Kaka yangu Mheshimiwa Shabiby amezungumzia tu mgogoro wa kwako kule pamoja na kwake. Kuna mgogoro kama huo wa Kiteto, mgogoro uliko baina ya Wilaya ya Chemba pamoja na Wilaya ya Kiteto ukiwa unahusisha hifadhi ya WMA-Makame. Wananchi wanakufa kule, hakuna vyombo vya habari vinavyoweza kuwamulika watu kwa namna gani wanavyokufa.
Mheshimiwa Spika, hayo matrekta yamechomwa moto hivi ninavyoongea, watu wameshapigwa, kuna watu 18 wameshafungwa jela, Mahakama ya Kiteto lakini kuna watu 27 wapo lock up Kiteto mpaka leo. Kwa hiyo, suala hili la migogoro tungeomba sana lishughulikiwe. Wabunge tuliambiwa tuorodheshe migogoro iliyoko katika maeneo yetu, tumeorodhesha migogoro hii kwa nchi nzima lakini hatupewi ripoti migogoro hiyo imesuluhishwa kwa namna gani na imeishia wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu aweze kuona suala la migogoro ya ardhi ndiyo itakayokwenda kutuletea vita ya wenyewe kwa wenyewe. Bila kumaliza migogoro ya ardhi ndoto za kufikia Tanzania ya Viwanda ni hadithi za Abunuwasi. Haitakuwepo kwa sababu ardhi hiyo ndiyo tunayoitarajia Watanzania wetu waweze kutafuta malighafi mbalimbali ili tuweze kuendesha hivyo viwanda ambavyo tunavisema leo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana mgogoro wa Kiteto pamoja na Chemba ambao unahusisha pia Makame-WMA ambayo iko Kiteto ambayo hifadhi ile inawanufaisha watu wa Kiteto basi ufanyiwe kazi kwa haraka ili wananchi wale waweze kupata maeneo yao ya kuweza
kulima na waweze kujijengea uchumi wa familia zao lakini na Taifa kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda ulioweza kunipatia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa machache niliyonayo kwenye Wizara hii muhimu ambayo inakwenda kuwahudumia Watanzania walio wengi. Kwa kuanza, nami naomba niungane na wenzangu kwenye suala zima la TARURA. Kwenye suala zima la TARURA nitaomba niende kwenye muktadha tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapitisha hapa hii taasisi ya TARURA, mwaka 2017, Serikali ilituhakikishia kwenda kutoa ushirikiano wa kutosha kwa watumishi wetu ili waende wakatimize wajibu na majukumu yao kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania. Hata hivyo, ninapata kigugumizi na sijui ni kwa nini? Serikali baada ya kuletewa TARURA ikatoa watumishi, wahandisi (engineers) waliokuwa kwenye Halmashauri ikawapandisha na kuwapa nafasi mbalimbali; Meneja wa Wilaya, Meneja wa Mikoa na Wakurugenzi. Baada ya kuwakabidhi majukumu hayo, watu hawa tunavyoongea mpaka leo hii, muda huu nimesimama, dakika hizi ninazoongea, watu hawa kuanzia Meneja wa Wilaya, Meneja wa Mkoa na Wakurugenzi wote, miaka minne kasoro hakuna hata mtu mmoja mwenye barua ya kuthibitishwa kazini kwenye nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu watu hawa wana barua za kukaimu. Wanakaimu miaka minne kasoro, lakini Serikali mpo, halafu ni Ofisi ya Rais, ambayo inakwenda kuhudumia Watanzania walio wengi kwenye Sekta muhimu inayokuza uchumi wa Taifa letu kutokana na kilimo! Mtu ambaye amethibitishwa kazini ni mtu mmoja tu, Mkurugenzi Mkuu wa TARURA, baba yangu Victor ndiye amethibitishwa kazini. Mtu ambaye alifanya kazi hii kwenye Taifa letu na ninatambua mchango wake mkubwa, amelitumikia Taifa lake, akastaafu, lakini akarudishwa tena kwa mkataba, yeye ndio mwenye barua ya kuthibitishwa kazini, wenzake wote wana barua za kukaimu mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Ummy, nakuamini katika uwajibikaji na uchapaji kazi. Kama tunataka kuwasaidia Watanzania na kukuza uchumi wa Taifa letu na watumishi wetu waweze kufanya kazi vizuri kwenye taasisi hii, naomba ukitoka hapa, kesho tunahitimisha bajeti yako, nenda kaanze na suala zima la kuhakikisha watumishi wetu wote wa ngazi ya Wilaya na Mkoa, Wakurugenzi wapate barua zao za kuthibitishwa kazini. Kama mnaona hawafai, waondoeni, tafuteni watu wanaofaa, wapeni mamlaka waweze kufanya kazi. Siyo kuwakaimisha watu miaka minne, ni kitu ambacho hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zinazokwenda kutokana na kukaimisha watu hawa na kutokuwa na mamlaka ya kwenda kutimiza wajibu na majukumu yao ripoti ya CAG inatuambia kutokana na udhaifu huo, TARURA kwa miaka mitatu mfululizo, nitaisema miwili tu mfululizo, imebaki na bakaa. Yaani fedha ambazo zimebaki bila kwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2018/2019 TARURA walibaki na bakaa ya shilingi bilioni 72.3 ambazo leo Wabunge tunapiga kelele humu ndani zingeweza kwenda kufanya kazi. Hakuna mtu wa kufanyia maamuzi, yuko mtu mmoja pale, kazi zimelala, fedha zinarudi, halafu bado sijui tunataka kufanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019/2020 shilingi bilioni 1.5 ziko pale, zimerudi. Barabara tunalalamika, miundombinu ni mibovu, wananchi wanakufa barabarani kwa kukosa huduma za barabara, akina mama wajawazito wanashindwa kwenda kujifungua watoto wao, wanajifungulia barabarani kwa sababu tu ya jambo dogo ambalo tunatakiwa tulisimamie ili watu wetu waweze kupata hiyo huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hebu twende tukafanye hii kazi ya kwenda kuwathibitisha hawa watu kazini ili tuweze kufanya kazi ya kulijenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala zima la posho za Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Vijiji. Tuna chaguzi mbili; tuna uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu. Madiwani tunafanya nao uchaguzi pamoja. Tukija kwenye suala la malipo tunawabagua Madiwani wakalipwe na Halmashauri kwenye mapato ya ndani, wakati watu hawa ndio tunaokwenda nao katika uchaguzi wetu. Ni kitu gani kinachosababisha Madiwani wetu wasiwekwe kwenye mfumo wa Serikali wa kulipwa mishahara yao na posho zao ili waweze kutimiza wajibu na majukumu yao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Madiwani leo ndio watendaji wetu wakuu kule chini. Sasa hivi tuko humu Bungeni, vikao vya Mabaraza ya Madiwani vinaendelea kule. Wao ndio wanaojua nini kinachoendelea kwenye kata zao, lakini watu hawa hawathaminiwi, tumewasahau. Namwomba Mheshimiwa Waziri na Serikali, tuone ni namna gani tunawatoa Madiwani wetu kuwaleta kwenye Serikali Kuu; mishahara walipwe na Serikali Kuu na vikao vyao pia vigharamiwe na Serikali Kuu ili tuachane na biashara ya kuendelea kuwakopa Madiwani kila mwaka na kila vikao na vikao vingine havifanyiki kwa sababu Wakurugenzi wanakuwa na kigezo cha kwamba hakuna fedha, kwa hiyo, siwezi kuitisha baraza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la Wenyeviti wetu wa Vijiji, Mitaa pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji na Wajumbe. Watu hawa nao pia ni watu ambao wanafanya kazi kubwa sana. Tukae tukijua Wenyeviti wa Vijiji pia ndio wanaoishi huko na ardhi zetu za vijiji ambavyo leo vimekuwa na migogoro mikubwa, chanzo kikubwa pia ni Wenyeviti wetu wa Vijiji kwa sababu hawana chochote mkononi.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanakwenda kule wanatafuta ardhi na Mwenyekiti akiambiwa bwana, Mwenyekiti mimi nina shilingi 50,000 hapa, wewe nikatie hapa kidogo tu. Mwenyekiti anaona sasa hii shilingi 50,000 wakati wewe umenisahau, nifanye nini? Anamkatia eneo pale, anachukua shilingi 50,000 yake, maisha mengine yanaendelea, tunakuja kurudi kwenye timbwili la kuanza kusuluhisha migogoro kwamba mimi nilipewa na Mwenyekiti wa Kijiji, huyu anasema hii ilikuwa ni hifadhi, huyu anasema vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Wajumbe wa Vijiji pamoja na Mitaa, watu hawa tukiwatoa Madiwani wakaenda Serikali Kuu, tuwarudishe Wenyeviti wetu wa Vijiji walipwe na Halmashauri kwa sababu tunakuwa tumeipunguzia Halmashauri mzigo wa kulipa Madiwani na hivyo waende wakaanze kuwalipa Wenyeviti wetu wa Vijiji kupitia mapato ya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la ahadi ya shilingi milioni 50 kila Kijiji. Uchaguzi wa mwaka 2015 kwenye Ilani ya Chama cha Mpainduzi mliwaahidi Watanzania kuwapatia shilingi milioni 50 kila kijiji ili waweze kukuza uchumi kwenye maeneo yao.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba ahadi iliyotolewa ilikuwa ya mwaka 2015 – 2020, nasi tulienda tukawaeleza wananchi juu ya jambo hilo kwamba tuliahirisha kufanya mambo mengine. Kwa hiyo, Ilani inayotekelezwa sasa ni 2020 - 2025. Kwa hiyo, hayo ya nyuma hayako kwenye tender hiyo sasa hivi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru naomba niendelee, nam-ignore tu Mheshimiwa Getere. Nimefunga, kwa hiyo, naomba aniache tu nisije nikatengua swaumu yangu. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaahidi wananchi wetu shilingi milioni 50 kwa ajili ya kwenda kuhuisha uchumi wao kwenye maeneo yao, lakini kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambaye yeye ndiye anaye-deal na vijiji vyetu, sijaiona hiyo milioni 50 humu. Nakumbuka mwaka 2017, nilichangia kwenye bajeti kuu ya Serikali na nikaambiwa…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mnzava.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe Taarifa mzungumzaji anayeendelea kwamba, ahadi ya milioni 50 ya kwenye ilani ya mwaka 2015 ilitekelezwa kwa namna mbalimbali ikiwemo kupeleka mikopo kupitia fedha za mapato ya ndani ya halmashauri. Kwa sababu ya utekelezaji wa namna hiyo ndio maana wananchi walikiamini tena Chama Cha Mapinduzi kikashinda kwa kishindo kwenye uchaguzi wa mwaka 2020. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Hizi ahadi kila ahadi ilikuwa inajitegemea. Waliahidi vituo vya afya, waliahidi maji kumtua mwanamke ndoo kichwani, waliahidi barabara ambazo wameshindwa kuwathibitisha hata watendaji wa TARURA na waliahidi milioni 50. Kwa hiyo, tunachokitaka nataka kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI milioni 50 ya kila Kijiji ambayo ilani yao hiyo, kama watakuwa wanaandika ilani kila baada ya miaka mitano wanasema hii ilipita hatuwezi kutekeleza tunaanza na mpya, Waheshimiwa basi kwa kweli, tusiendelee kuwaibia Watanzania kwa style hii, lakini kama tunaendeleza yale yaliyokuwa yamebaki…

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hii itakuwa Taarifa ya mwisho. Mheshimiwa Agness Mathew Marwa.

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa Taarifa kwa muongeaji kwanza anatoa lugha ya maudhi, lakini kingine anatakiwa ajue kwamba, mpaka sasa hivi muda bado. Mama atayatekeleza yote, kwa hiyo, aache kashfa. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti malizia sekunde zako chache zilizobaki.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikushukuru. Hata ninyi wenyewe mmepoteana huko, yaani hamjui nini ambacho mnakifanya, kwa hiyo, mimi niwashauri tu na najua Mheshimiwa Mama Samia ni mwanamke ambaye anaweza kusimama na anasimama. Nina hakika atakuwa amenisikia na atakwenda kuwapoza Watanzania hiyo milioni 50 ili isiwe ahadi ya uwongo. Naye tunamwamini na mwanamke siku zote akimuahidi mtoto wake kwamba, nitakuletea pipi, basi akitoka akirudi anakuja na pipi, atakwenda kutekeleza hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dakika chache ama sekunde chache zilizobaki, naomba niendelee na suala zima la mikopo ya akinamama, vijana na watu wenye ulemavu kama wenzangu walivyosema. Mikopo hii kwenye halmashauri zetu nyingi imekuwa ni mikopo kichefuchefu naweza nikasema. Kwanza vikundi vinavyokopeshwa vina walakini na vikikopeshwa fedha hizo hazirudi, zikichukuliwa zimechukuliwa jumla. Ukihoji hakuna maelezo yoyote ya kina ya kutosha yanayokwenda kutoa majibu kuhusiana na mikopo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hii tulisema tuwapatie wanawake wetu na vijana na watu wenye ulemavu ili kuweza kupunguza familia tegemezi ambazo Serikali imekuwa ikiendelea kutoa mchango kwenye kupitia mfumo wa TASAF kwenda kuzisaidia familia tegemezi ama familia maskini. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara ya TAMISEMI iweze kuona na kufuatilia suala zima la mikopo hii ya asilimia 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa muda wako na Mungu akubariki sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti hii ya pili ya Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali ambayo mwaka jana wakati tunachangia bajeti humu ndani ilijinasibu sana na tukawa tunaambiwa Waheshimiwa Wabunge tulieni bajeti ni ya kwanza.

Mimi jinsi ninavyoamini kati ya awamu zote zilizopita na zinazoendelea naweza nikasema kuwa, awamu itakayofanya vibaya na Watanzania watakuja kulia sana ni Serikali hii ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnawaahidi Watanzania mnaacha kutekeleza mliyoyaahidi mnakuja mnatekeleza mambo tofauti na vile mlivyoahidi, yaani mnaimba kama malaika mnakuja kucheza kama mashetani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mliwaahidi Watanzania kuwajengea barabara….

TAARIFA .....

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru kwa kuweza kuniruhusu niweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, wakati wagombea wakijinadi na vyama mbalimbali vikijinadi kwa Watanzania, vilikuwa vinanadi mambo mbalimbali ama shughuli mbalimbali za kijamii ambazo vyama hivyo


vitatekeleza kama vitapewa ridhaa.Mliwaahidi Watanzania kuwajengea barabara ili ziweze kupitika kwa mwaka mzima kipindi cha masika na kipindi cha kiangazi, hamjajenga barabara hata moja, mnawapelekea Watanzania waende wakawalipie motor vehicle.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hujajenga barabara unaenda unampelekea mwananchi wa kijijini akakulipie motor vehicle na Wabunge mko humu ndani mnapiga makofi, wananchi wenu kule vijijini barabara zisizopitika kipindi cha masika waende wakalipe hii motor vehicle hii siyo sawa, kwenye Ilani ipi ya Chama cha Mapinduzi mstari upi, ukurasa gani uliandika kwamba mtaenda kuwalipisha Watanzania motor vehicle. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii motor vehicle mmeamua kwenda kuwapelekea Watanzania kwa kupandisha mafuta ya taa, diesel na petrol yaani leo Watanzania wa nchi hii, umeme ni anasa, walibakia na mafuta ya taa, nayo mafuta ya taa yanaenda kuwa anasa kwa Watanzania. Mnaturudisha enzi za huko nyuma zama za kale za kwenda kuanza kutembea na vijinga kwenye vyumba kwa nini tunawafanyia Watanzania vitu vya namna hii ninyi? Hivi kwa nini hamna moyo wa huruma! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapokwenda kupandisha mafuta ya taa wakati umeme umeshindwa kuwafikishia Watanzania unakwenda kuendeleza kumdhoofisha Mtanzania maskini aendelee kuwa maskini mpaka siku yake ya kufa, hii inajidhihirisha kuwa viongozi wa Chama cha Mapinduzi pamoja na Ilani yenu inajidhihirisha kuwa hamjawahi kuwa na dhamira ya dhati ya kwenda kuwaondoa Watanzania kwenye umaskini na ndio maana mnachokiadi hamtekelezi na mnajua mkitekeleza watu hawa wakiwa na uwezo wakawa na uchumi wao kwa story zenu hawatawachagua, kwa hiyo, mnabakia kila siku mnaahidi hiki mnaenda kutekeleza kitu kingine ili baada ya miaka mitano ikiisha mrudi tena kwenda kuahidi namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili suala la


kwenda kuhamisha motor vehicle kuwapelekea Watanzania waende wakalipe si sawa, si sawa kuwahamisha yaani motor vehicle ya Kunti nimpelekee mtu mwingine kule kijijini aende akanilipie motor vehicle, kila mmoja aende atimize wajibu na majukumu yake, Watanzania wale hawajatutuma sisi tununue magari, ni Watanzania wangapi wenye magari? Watu wengi waliopo vijijini hawana magari kwa hili suala nadhani halikai sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona Wabunge mnasema kwamba eti ile shilingi 40 iende kwenye maji, unakumbuka tulipendekeza hapa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji tulisema tutoe shilingi 50 iende kwenye maji, leo mnasema 40 iende kwenye maji, aliyewaambie inaenda kwenye nani? Nani aliyewaambieni inaenda kwenye maji? Hii inapelekwa badala ya motor vehicle, motor vehicle itakatwa kule tukinunua mafuta ndio umelipa motor vehicle, kwa hiyo, hili suala si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la kodi ya majengo, Watanzania hawa wanajenga kwa shida kweli, lakini kitu cha kwanza Mtanzania huyu analipa kodi ya ardhi, Mtanzania huyu analipa kodi kwenye cement, kwenye nondo, kwenye bati, kwenye kila kitu mpaka mchanga anaochota ardhini ukisombwa pale anaulipia kodi, leo tena hivi vijumba vyao ambavyo wamejijengea kwa shida mnaenda tena kuwanyonya hawa Watanzania waende wakawalipieni tena kodi, tena mnaenda kuwapandishia kutoka shilingi 3,000 mpaka shilingi 10,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawataka nini hawa Watanzania wa watu yaillai toba maulana, wametukosea nini Watanzania? Hivi kuwapa ridhaa ya kuongoza nchi hii ndio imekuwa adhabu kwao? Waoneeni huruma hawa Watanzania, mlienda kuwapigia pushapu mpaka misamba ya suruali ikachanika, kwa hiyo, waoneni kwamba ile huruma waliowapeni basi hebu itumieni kuweni na moyo wa huruma kwa binadamu wenzenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kodi ya majengo si


sawa, mngekuja mimi nilikua najua hapa mngekuja mkasema kwamba kama mnataka kodi ya majengo basi vifaa vya ujenzi vipinguzwe kodi ama viondolewe kabisa, ili muweze kuchukua hiyo kodi ya majengo, hamtoi vifaa vya ujenzi vinapanda kwa kupandisha mafuta vifaa vya ujenzi vitapanda. Lakini pili mnawapandishia hivyo vifaa vya ujenzi mnakwenda tena mnawatoza na kodi za majengo huko waliko, jamani mnawakamua kiasi hiki wamewakosea kitu gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu shilingi milioni 50, ni suala lile lile tunaimba kama malaika tunacheza kama mashetani, mliahidi hapa na mwaka jana tulisema, hili suala la milioni 50.

TAARIFA .....

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mdogo wangu Mariam nimsamehe bure tu, Jimbo lenyewe la Chemba halijui huyu, hiyo barabara imepita wala wananchi wa Chemba hawanufaiki na chochote kwenye lile Jimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Chemba, tulieni ninyi nini mnachozomea kitu gani? Tulieni hiyo, vitulizeni taratibu cristapen iingie, vitulizeni visiwashe saa hizi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina dakika zangu tatu zimebaki naomba unilindie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la shilingi milioni 50, mliwaahidi Watanzania kila kijiji kuwapatia shilingi milioni 50, tunataka tujue shilingi milioni 50 ni lini au ni deni watakuja kuwadai waanzie wapi kudai shilingi milioni 50, hatujaziona kwenye kitabu cha Waziri humu shilingi milioni 50 ziko wapi? Mlijinasibu na shilingi milioni 50 leo mwaka wa pili, bajeti ya pili hii kitabu kinapita empty, hata dalili wala harufu wala sisikii Mbunge wa CCM akiongelea suala la shilingi milioni 50, ni lini hizo shilingi milioni 50 mtazitoa?

TAARIFA.....

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nahisi Waheshimiwa Wabunge wa Chama cha Mapinduzi hawanielewi. Nimesema hivi jamani mlichokiahidi sicho mnachokitekeleza ni miaka miwili sasa, mliahidi shilingi milioni 50, mliahidi barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeahidi shilingi milioni 50 mmeenda kujenga uwanja wa Chato wa ndege! Hivyo ndiyo vitu shilingi milioni 50 mtaitoa lini? Siyo suala kwamba miaka Mitano, hivi vingine havikuwepo hata kwenye Ilani yenu, vimepatikanaje? Halafu unakuja unaniletea story hapa eti Ilani ya Chama cha Mapinduzi inanihusu nini mimi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Waziri akija hapa atuambie, shilingi milioni 50 ni lini zinaanza kutolewa kwa Watanzania wetu, ukidai ujue na kulipa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuweza kupata fursa ya kuchangia Wizara ya Ardhi, Maendeleo ya Makazi. Naomba nianze kuchangia Wizara hii, kwenye suala zima la migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hili la migogoro niseme tu Mheshimiwa Lukuvi amepata pongezi nyingi, lakini kwa Mkoa wa Dodoma kwa kweli kazi bado anayo. Nasema kazi bado anayo kwa sababu Mheshimiwa Lukuvi, atasema mambo kadhaa nitakayoyazungumza hapa hayahusiani na Wizara yake, lakini yeye ndiye tunajua Wizara yake inahusika na suala zima la makazi, bila ardhi makazi hayapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa yetu ya Dodoma, kuna kitu ambacho kinataka kuja kutengenezwa kinachofanana na kinachokuja kutengenezwa hapa KDA. Sisi Dodoma tuna msalaba unaitwa CDA, hii CDA ilianzishwa mnamo mwaka1973 kwa madhumuni na malengo ya kwenda kuhamisha Makao Makuu ya Serikali kuja Manispaa ya Dodoma ama Mkoa wa Dodoma. Yapata leo miaka 43 makao makuu yapo ya chama tu, ya Serikali hayapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize Serikali mko hapa team nzima, huyo Waziri Mkuu yuko hapa mwakilishi wake, lakini Wizara mbalimbali ziko hapa. Wana Manispaa ya Dodoma wanataka kujua, kama suala zima la uanzishwaji wa kitu kinachoitwa CDA, ilikuwa dhumuni lake na malengo yake ni kwa ajili ya kuleta, Makao Makuu Dodoma imeshindikana, kwa nini hii CDA isirudi Dar es Salaam ambako ndiko kuna makao makuu ya nchi? Badala yake kuendelea kuwatesa na hao Watanzania wasio kuwa na hatia yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, CDA ilikuja ili ipange mji wetu vizuri, igawe viwanja vyetu lakini pili, iweze kuwapatia wananchi wa Manispaa ya Dodoma ardhi, waweze kuiendeleza, waweze kupata makazi yaliyo bora. Leo wananchi wa Manispaa ya Dodoma, hawana ardhi ambayo wamemilikishwa na CDA badala yake wamegeuzwa kuwa watumwa ndani ya wilaya yao, wanaitwa wavamizi kila kunapokucha wanabomolewa nyumba zao. Inasikitisha sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi, wananchi hawa bila huruma CDA imekuja tangu mwaka 1973 kuna watu walikuwepo tangu mwaka 1959 kabla hata ya Uhuru. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Njedengwa pale walienda kuwavunjia watu wakampa eneo mtu mmoja tu, anaitwa Maimu, wakavunja nyumba 127, wakampatia maekari mtu mmoja anaitwa Maimu pale. Wananchi wetu wakawaacha hewani, wanateseka halafu leo wanataka kuendelea kuwashawishi Watanzania wa Manispaa ya Dodoma wabaki na CDA, hawaitaki CDA chukueni pelekeni kwenu, mnakoona kunafaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro hii nimeona hapa kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri, migogoro iliyoripotiwa ni migogoro miwili tu, (d) center na (c)center, si kweli. Nami nimshukuru Mheshimiwa Waziri hili begi lake alilonipa nimeweka haya ma-document ya CDA, ya wananchi haya, yako humu yamejaa haya humu, haya nimemletea. Mimi hili begi kazi yake nitakuwa nabeba makablasha ya wananchi, wanaoandika barua kwenye Ofisi zenu hamuwajibu, mnaitetea CDA, mnaenda mnakaa kwenye vikao vya Bodi ya CDA mnawaangamiza Watanzania wa Manispaa ya Dodoma, wamewakoseeni nini? Kwa nini mnawanyanyasa hawa watu kiasi hiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapimieni ardhi, wapeni ramani zenu, wapeni waende wakajenge, watu wanahangaika barabarani wanauza machungwa akinamama wajane, wana watoto wanasomesha, wanakwenda wanajijengea nyumba zao, mnaenda mnawavunjiwa, mnawaambia wavamizi. Mnachotaka ni nini, kuwaua? Waueni basi tujue moja kama hamuwataki, watu hao hao ndiyo wanaendelea kuwasitirini ninyi kupata kura, halafu bado mnaleta blabla hapa, za kuendelea kuwanyanyasa namna hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, safari hii mlipiga magoti na kupiga push up mwaka 2015 mwaka jana, 2020 nahisi mtaruka kichura chura. Kwa sababu hawa watu hawako tayari kuendelea na mateso haya na mwakilishi wa Waziri Mkuu aliyeko hapa, wananchi wa Kata zote 41 za Manispaa ya Dodoma, wanahitaji kukutana na ofisi ya Waziri Mkuu, ili waeleze manyanyaso na mateso wanayoyapata na hawa watumishi wa CDA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, CDA haisimamiwi na mtu yeyote ipo tu ina-hang hapo, inajifanyia mambo inavyotaka, inafunga ofisi tarehe 2 Februari, wamefunga ofisi eti kisa mfagizi kafiwa na mume wake, sisi mbona huwa hatuahirishi Bunge hapa mama yangu Stella amefiwa, mbona hatujaahirisha Bunge ili twende tukamzike mama yake Stella. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mume wa mfagizi wa CDA kafiwa wamefunga ofisi ambayo inahudumia zaidi ya watu 40,000 kweli ni mateso gani mnayowatesa hawa watu. Wana kikao tu cha kawaida cha kikazi wanafunga ofisi eti wamekwenda kwenye kikao, hawa watu kwa nini mnawaendekeza kiasi hiki? Hiki kiburi mnawapa ninyi Serikali. Laiti mngeamua kuwasimamia na mkawaambia lengo na madhumuni ya kuanzishwa kwa CDA wangeshika adabu, wangefuata Kanuni na taratibu za nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wetu wanakwenda wanachukua ardhi zao, wakichukua ardhi badala ya kwenda kuwafanyia maboresho ya ardhi pale wawapimie watu mahali walipo, hawawapimii mahali wanawaambia tunapima upya. Wanawafukuza kwenye maeneo yao, wanaenda wanapima vile viwanja, wakipima viwanja wanawalipa fidia laki tano, kiwanja kinaenda kuuzwa milioni tano ama milioni nane, mwananchi gani anaenda kupata hiyo milioni nane ya kununua kiwanja. Ardhi umemkuta nayo mwenyewe, wana mashamba yao yaliyokuwa enzi na enzi, walikuwa wanayatumia kulima ardhi ya Dodoma hii haiongezeki inapungua, ila watu tunaongezeka. Kwa hiyo, ni lazima CDA muiambie na itambue, kwamba wanahitaji siku ngapi wakamilishe upimaji wa ardhi Manispaa ya Dodoma wafungashe vilago vyao waende wanakotaka kwenda, sisi Dodoma hapa tumechoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawawezi kufanya hiyo kazi, Mheshimiwa Lukuvi na Waziri Mkuu, wananchi wa Dodoma watakachokuja kukifanya wasije wakaleta lawama, wamechoka kunyanyaswa na mateso ya CDA. Hilo nimemaliza kwenye CDA, naomba lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wangu wanataka kukutana na Waziri Mwenye dhamana na Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa sababu Wabunge wa Majimbo hususani Jimbo la Dodoma Mjini, mmekuwa mkiwafunga midomo wasisemee suala la CDA. Alianza hapa Malole mwaka juzi mkamfunga zipu, eti ooh usiongee kwani ni ya nani, kama ni ya kwenu si mseme, kama na ninyi mnanufaika humo semeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Migogoro ya Swagaswaga ambayo najua iko kwa Mheshimiwa Maghembe, lakini suala lile la Swagaswaga, Mkungunero Dagram A mgogoro wa uliopo katika mpaka wa Chemba na Kiteto. Tunahitaji mpaka ule Waziri akautatue. Bunge la mwezi wa Pili, wazee wa watu walitoka Wilaya ya Chemba, wakaja kumwona Mheshimiwa Waziri wakamwelezea hali halisi iliyoko pale kati ya mgogoro wa Chemba na Kiteto, Mheshimiwa Waziri hata ile wakawapa maneno matamu, wakawarudisha wazee wa watu na wakawaahidi Waziri Mkuu anakwenda. Mpaka leo Waziri Mkuu hajawahi kukanyaga, wala harufu tu ya kusikia kwamba atakuja kwenda haipo, kwa nini wanawadharau hawa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawawezi kushughulikia, wawambie wajichukulie hatua wenyewe watajua nini cha kufanya huko, mpaka wasubiri watu wafe ndio wataona ving‟ora na magari 42 yanafukuzana yanakwenda kuangalia maiti za watu kule. Kwa nini mnafanya namna hii ninyi? Wananchi wa Dodoma wamewakoseeni nini? Tuambieni kama kuna makosa ambayo tumewakosea tuwaombeni radhi, ili na sisi tuweze kupata haki ya kuhudumiwa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kama maeneo mengine.
Maeneo mengine umefanya, Dodoma kwetu wewe ni sifuri na mbaya zaidi ulikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma hii, usichokijua ni nini wewe Mheshimiwa Lukuvi, kipi usijchokijua kwa Dodoma hii ambayo umekaa kimya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante ni mzuka tu! Suala la nyumba huko Swagaswaga na wapi huko niwaombe tu mwende wananchi wale, wazee wa watu wanalalamika huko, dharau hawazihitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba, wakati Kamati zinaundwa nilikuwa mjumbe wa Kamati hiyo kabla sijabadilishwa, nilikwenda kuona nyumba zinazojengwa na Shirika la Nyumba, nyumba zile sijui maana yake tulipoziona zilikuwa hazijaisha lakini tukaambiwa zikiisha zitakuwa nzuri, sasa sijui zinakuwaje nzuri kabla ya kwisha sijaelewa, chumba kinachokwenda kuwekwa mtu pale ukiweka kitanda cha futi tatu na nusu, utaweka na meza ndogo ya kuwekea mafuta ya kupaka, labda na kitana na dawa ya mswaki. Chumba huwezi kuweka kitanda cha tano kwa sita, nani siku hizi analeta biashara ya mbanano kwenye vyumba, vyumba vya kulala havina hadhi…
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana.
MHE. KUNTI Y. MAJALA Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango huu haujaonesha baadhi ya sekta katika kukuza pato la Taifa:-
(i) Sekta ya madini
(ii) Sekta ya Maliasili na Utalii
(iii) Bandari
(iv) Gesi
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kufahamu sekta ya madini itachangia kiasi gani? Hisa za Serikali katika miradi ya uchimbaji madini kwenye migodi ya Geita, Mwadui, Buzwagi, Tanzanite One na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika nchi yetu, uchimbaji wa gesi umeanza lakini katika mpango huu haujaonyesha ni kwa namna gani sekta hii itaongeza pato la Taifa. Pia ningependa kujua ununuzi wa vitalu mpaka sasa ni vitalu vingapi viko mikononi mwa wawekezaji na vinaingiza shilingi ngapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huu haujaonyesha sekta ya maliasili ina malengo kiasi gani. Napenda kujua mchango wa Serikali katika mpango huu wa 2017/2018. Kwenye upande wa Bandari pia uko kimya ni kwamba Bandari ndiyo inakufa?
Mheshimiwa Naibu Spika, ili tufike kwenye Tanzania ya viwanda ni lazima tuwekeze kwenye kilimo na siyo kilimo tu. Tunahitaji kilimo cha kisasa ili tuwe na malighafi kwa ajili ya viwanda. Pia kwenye mpango huu kilimo alichokitaja Mheshimiwa Waziri upande wa mazao ni mazao ya chakula tu. Ushauri wangu, tuongeze mazao ya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, Afya; ndani ya nchi sasa madawa yamekuwa tatizo, tusipoongeza fedha upande wa afya ni dhahiri kuwa katika viwanda tunavyotarajia kuvijenga tutaendelea kuajiri watu toka nje, hivyo tuna kila sababu ya kuboresha hospitali zetu ili tuwe na jamii yenye afya bora.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kupata nafasi na mimi ya kuweza kuchangia Wizara hii ya Maji. Kwa kuwa dakika chache lakini Wizara hii nyeti naomba niende moja kwa moja kwenye kitabu cha Waziri na bahati nzuri mimi nina vitabu viwili vyote, cha mwaka jana na kitabu cha mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa Ntomoko ambao niliusemea pia katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Mradi huu wa Ntomoko unabadilishwa tu maneno kwenye vitabu vya Mheshimiwa Waziri. Kitabu cha mwaka wa jana alituletea mradi wa Ntomoko kwamba unahusisha Halmashauri mbili za Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa. Kitabu cha mwaka huu hali ya huduma ya maji kutoka chanzo cha Ntomoko imeshindwa kukidhi mahitaji na kupunguza vijiji, yaani tunabadilishiwa maneno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mradi huu Mheshimiwa Waziri unalifahamu vizuri. Mradi wa Ntomoko ni disaster, haiwezekaniki. Leo mnakuja kutuandikia hapa ilhali mnajua kabisa nini kinachoendelea kuhusiana na suala zima la Ntomoko. Mheshimiwa Waziri, suala hili kama mnashindwa kuwawajibisha watu ambao wameweza kutenda dhambi kwa Watanzania wenzao kwa kupoteza fedha nyingi shilingi bilioni 2.4 wamezilamba, maji hakuna, wananchi wanapata shida ya maji, mna kazi ya kutubadilishia maneno kwenye vitabu, hatuwatendei haki wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hela zile si hela ambazo watu wale wanaomba, fedha ile wananchi wa Wilaya ya Chemba na wao ni miongoni mwa Watanzania wanaolipa kodi, wanatakiwa wapate hii huduma muhimu ya maji. Wilaya ile ina shida ya maji haijapatikana kuona. Kituo cha Afya cha Hamai hakina maji, nilisema, mwaka jana niliwaambia Wizara, mnaendelea kutubadilishia maneno kwenye hivi vitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja, naomba aniambie suala la Ntomoko hatma yake ni nini? Wananchi wa Chemba tumesema huu mradi hatuutaki kaeni nao ninyi, tutafutieni mradi mwingine ambao tutapata maji. Hamuwezi kuwa mnaendelea kutubadilishia vijiji vyote, kata zote 26 hakuna maji. Mlitupa hivyo vijiji kumi navyo vimekuwa shida hakuna maji, mnataka nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya maeneo ambayo mnaendelea kufadhiliwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni miongoni mwa Mkoa wa Dodoma ndimo mnamopata kura humu, lakini bado hata hamuwakumbuki watu hawa, kwa nini mnafanya namna hiyo? Waswahili akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli. Sasa kama rafiki huyu mnamuona hana maana atakapokuja kupata rafiki mwingine msije mkamlaumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la maji DUWASA. Sijaona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri kikiniambia kwamba kutokana na ujio wa Makao Makuu kuhamia Manispaa ya Dodoma ambayo ndiyo itakayobeba watu wengi, sijaona mpango mkakati wa upatikanaji wa maji katika Mji wa Dodoma. Tuna kata 41 katika Manispaa ya Dodoma, ni kata 18 tu ndizo zina maji; na katika hizo kata 18 haizidi mitaa 50 ambayo inapata maji katika hizo kata 18. Sasa tuna huu ujio, Mheshimiwa Waziri hujatuambia nini mkakati wa Serikali kuhakikisha maji yatapatikana pamoja na ongezeko kubwa la watu linalokuja kuingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, DUWASA hii ina majanga ya madeni kwenye taasisi za Serikali, na naomba nizitaje na utakapokuja hapa Mheshimiwa Waziri naomba uniambie madeni haya yatalipwa lini na taasisi za Serikali. Inakuwa ni aibu na ni masikitiko makubwa sana mwananchi wa kawaida anakatiwa maji, hapati maji mpaka alipe bili ya maji, taasisi za Serikali hamtaki kulipa maji mnadaiwa mabilioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, DUWASA inadai shilingi bilioni 1.9; kati ya hizo Jeshi la Polisi linadaiwa shilingi milioni 600, Magereza shilingi milioni 200; JWTZ inadaiwa shilingi milioni 100, JKT shilingi milioni 500, Makamu wa Rais… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu, Wizara ya Ujenzi ambayo inahusisha barabara zetu pamoja na viwanja vyetu vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala zima la ulipaji wa fidia kwa wananchi wetu wanaokwenda kupisha maeneo yanayokwenda kujengwa viwanja vya ndege, lakini pili na barabara zetu. Wizara ya Ujenzi kupitia Mamlaka ya Uwanja wa Ndege Dodoma, Airport hii hapa iliwasimamisha wananchi wa eneo la Makole tangu mwaka 2016 mwezi Mei wakiwa wanahitaji maeneo yale kwa ajili ya kupanua uwanja wa ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja ule wananchi wale waliosimamishwa baadhi walilipwa lakini wengine waliobaki zaidi ya wananchi 57 mpaka leo hawajalipwa fidia na wamezuiliwa kuendeleza makazi yao na hakuna tamko lolote linaloendelea, wamebaki wako pale nyumba zinapata ufa, hawawezi kupaka rangi, hawawezi kufanya chochote, wameshabomoa na wameshaweka uzio tayari. Wizara ya Ujenzi kupitia kwa Mheshimiwa Waziri atuambie wananchi wale waliobaki kwenye Uwanja wa Ndege, Airport hii iliyoko hapa Makole, ni lini watalipwa fidia zao ili waweze kuondoka eneo lile na kama hawalipwi hawaoni sasa ni wakati wa kwenda kuwaruhusu waendelee na ukarabati wa makazi yao na kuwapa kibali cha kuendelea kuishi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hilo, kwa kuwa wamewachelewesha, waliwafanyia tathmini ya kuwalipa fidia tangu mwaka 2016 mwezi Mei, wamewakalisha muda wote zaidi ya miaka mitano, sita sasa; watakapokwenda kuwaruhusu kuishi kama hawawalipi fidia ya kuwaondoa hawaoni sasa kuna sababu pia ya kuwalipa kifuta jasho kwa kupoteza muda wao mrefu na kushindwa kuendeleza makazi yao hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna Uwanja wa Ndege wa Msalato hali kadhalika uwanja ule na wenyewe kuna wananchi waliotakiwa kupisha ujenzi wa uwanja ule, walilipwa zaidi ya wananchi 200 wakabaki wananchi 89; tangu mwaka 2011 mpaka leo wananchi hawa hawajalipwa. Pia nataka kujua wananchi hawa wanalipwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na ulipwaji wa fidia, nimeona hapa kwenye kitabu cha Waziri anasema uwanja huo wa ndege uko kwenye mchakato. Mchakato mpaka lini, zaidi ya miaka 10 kiwanja hiki ni mchakato tu. Waziri akija kuhitimisha hoja yake jioni ya leo, naomba kujua ni lini sasa kwa tarehe ili tuweze kujua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dodoma wa Msalato unakwenda kuanza ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala zima la barabara zetu. Nitazungumzia barabara moja muhimu sana kwa maslahi mapana ya wananchi wa mikoa minne. Tunafahamu fika barabara ndiyo uchumi wa Taifa letu. Bila barabara hauwezi kupata huduma ya afya au huduma yoyote ya msingi au kufanya shughuli zozote za kibinadamu. Tuna barabara ya kutoka Kilindi - Kiteto – Chemba (Dodoma) - Singida.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii iliahidiwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa; miaka 10 imeisha barabara haijajengwa. Akaja Rais wa Awamu ya Nne akaahidi barabara hii kujengwa kwa kiwango cha lami; miaka 10 imepita barabara hii haijajengwa. Akaja Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ikawekwa kwenye Ilani ya CCM mwaka 2015 - 2020 imepita bilabial. Imewekwa kwenye Ilani ya mwaka huu 2020-2025, kwenye kitabu cha Waziri inasema barabara hii inakwenda kufanyiwa upembuzi yakinifu; miaka 25 Ilani ya Chama cha Mapinduzi mnafanya upembuzi yakinifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo si sawa. Sisi wananchi wa Wilaya ya Chemba barabara pekee inayoweza kukuza uchumi wa wilaya yetu ni barabara ya kutoka Kilindi kuunganisha na Mkoa wa Singida. Kati ya kata 26 za Jimbo la Chemba; kata 12 ndizo zilizopitiwa na barabara hii. Tukijenga barabara hii kwa kiwango cha lami tutakwenda kukuza uchumi wa wilaya yetu kwa kuwa …

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa inatoka wapi sioni Mbunge akisimama. Waheshimiwa Wabunge ukisema neno taarifa inabidi usimame ili nikuone. Mheshimiwa Eng. Ulenge.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba tu kumpa taarifa mzungumzaji nafikiri ana lag behind the information. Barabara anayoitaja inakwenda kujengwa kilomita 20 na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi alitamka hapa Bungeni; Phase I ilikuwa ni kilomita 50 lakini kutokana na scarcity ya bajeti kilomita 20 inakwenda kuanza kujengwa. Sisi watu wa Tanga tunaifuatilia kwa karibu kwa sababu ni muhimu kwa uchumi wa Mkoa wa Tanga. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niendelee kwa sababu yeye anazungumza biashara ya kilometa 20; kwako Tanga kuna lami mama sisi Chemba hatuna lami. Kwa hiyo, ukiniambia biashara ya kilometa 20 none of my business. Kwanza, hata hiyo kilometa 20 imeanza au iko tu kwenye maandishi? Bunge la Kumi na Moja tuliambiwa inakwenda kujengwa, haikujengwa. Kwa hiyo, tunachokitaka hapa na nachotaka kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kama barabara viongozi wetu wakuu wa nchi wanaahidi awamu zote mbili kipindi cha Awamu ya Tatu, Awamu ya Nne, miaka 20 hamjajenga barabara leo mtu anakuja kuniambia kwamba wanajenga kilometa 20, so what? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii sisi Wanachemba na Mkoa wa Dodoma ndiyo itakayokwenda kutusaidia kujenga uchumi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba. Serikali imekuwa ikisema humu ndani kwamba Halmashauri ambazo zitakuwa na uchumi mdogo au zitakazoshindwa kukusanya mapato zitakwenda kunyang’anywa; sisi Chemba hatuna chochote tunategemea kilimo, wakulima wetu wanaolima Wilaya ya Chemba, tunatarajia tuwe na miundombinu rafiki kuwezesha kuuza mazao ili tuweze kukuza uchumi wa Halmashauri lakini hatuna barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wafanyabiashara wa mazao wanakuja kununua mazao kwa wakulima wetu kwa bei ya chini kwa sababu ya miundombinu mibovu ya barabara. Wawekezaji wanashindwa kuja kuwekeza ndani ya Wilaya ya Chemba kwa sababu miundombinu ya barabara si rafiki atakuja kuwekeza ili afanye nini? Sisi tuna mapori mawili; (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Mkungunero na Pori la Swagaswaga, tunaweza kupata watalii kama tutakuwa na barabara hii ambayo itatusaidia kuendelea kujenga uchumi wa Halmashauri yetu. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atakapokuja biashara hii ya kilometa 20, tutashughulika humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu jana walikuwa wanasema kuna upendeleo na ukiangalia ni kweli; kata 26 huna barabara ya lami hata kilometa moja halafu unasema uko sawa, kweli? Hata watoto nyumbani mzazi ukimnunulia huyu leo kaptura, kesho mnunulie mwingine, inakuwaje mtoto huyo huyo kila siku ndiye unayemnunulia kaptura halafu mwingine unamuangalia? Kwa akili ya kawaida kama binadamu atahisi yeye kabaguliwa au katengwa na mwisho wa siku mtoto yule ataanza kuishi maisha ya kujitenga. Hatuhitaji ndani ya Bunge hili na ndani ya Taifa letu tuanze kuonekana kwamba kuna mikoa ambayo yenyewe ndiyo mizuri zaidi na inastahili sana na mikoa mingine ambayo haistahili.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sera ya Wizara ya Ujenzi inakwenda kuunganisha barabara za mikoa kwa mikoa na wilaya kwa wilaya. Tuna barabara ya kutoka Mrijo Olboloti, inapita mpaka daraja la Simba Kelema tunaunganisha na Wilaya ya Kondoa. Kuna daraja pale lilikatika mkaenda kuwaambia eti TARURA ndiyo waende wakajenge daraja lile, TARURA ana uwezo wa kujenga daraja la namna gani? TARURA mnaowapa bajeti ya 30% TANROADS wanachukua 70%, TARURA wataweza kujenga daraja lile? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja aniambie daraja lile la Kelema Simba Maziwani ni lini litakwenda kujengwa la uhakika ili tuondokane na adha ya Watanzania wetu wa Wilaya ya Chemba kusafiri kwa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna eneo lingine korofi sana; kuna eneo la Mto Bubu ambao unapita Kata ya Songolo, wakati wa kipindi cha mvua maji pale huwa yanajaa kweli kweli na abiria wanaposafiri wakikutana na ule mto ni lazima wasimame ili mto upite na wao waweze kuweza kupita. Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha naomba atuambie maana wananchi wa Wilaya ya Chemba tunahitaji Daraja la Songolo ili kuokoa maisha ya wananchi wetu na watoto wetu wa shule kwa sababu tuna shule ya msingi na sekondari ambapo mwaka jana watoto wawili; mmoja wa sekondari na mwingine wa shule ya msingi walifariki kwa kusombwa na maji kutokana na lile daraja pale maana wanavuka kwenda shuleni.

Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja pia atuambie nini anachokwenda kufanya kuhusiana na daraja hili, hata kama ni la dharura tutengenezeeni wakati mnaendelea kujipanga ili muweze kutuwekea daraja linalostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa machache haya, nakushukuru kwa muda wako lakini fidia Uwanja wa Ndege wa Airport pamoja na Msalato naomba kujua hatma yake. Pia naomba kujua hatma ya kilometa 461 za barabara ya kutoka Kilindi mpaka Singida zikiwa zinapita Chemba. Nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na mimi kunipatia nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Awamu ya Sita ambayo tunaianza mwaka 2021/ 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kuipongeza Serikali. Tangu lilivyoingia Bunge la Kumi na Moja kilio changu kilikuwa ni malipo ya Madiwani kupelekwa Serikali Kuu, hata wakati nachangia Wizara ya TAMISEMI nilisema kwamba tunaomba Madiwani wetu wakalipwe stahiki zao na Serikali Kuu ili kuwaondolea mzigo wa kukopwa…

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naomba tupunguze sauti tuwasikilize wachangiaji.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweze kuwalipa Madiwani wetu kupitia Serikali Kuu ili kuwapunguzia mtihani na msalaba mzito waliokuwa wanaubeba Madiwani kwa kukopwa na Wakurugenzi kwenye halmashauri zao. Kwa hiyo niwapongeze sana, na niipongeze sana Serikali kwa kuliona hilo na kuweza kuwapelekea Madiwani kwenda kuwalipa kwenye Serikali Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipendekeza hapa wakati nachangia Wizara ya TAMISEMI, kwamba Serikali ikipeleka Madiwani wetu kwenda kulipwa Serikali Kuu tuna watu hawa ambao pia wao ndiyo watendaji wetu wakuu huko chini baada ya Madiwani. Wenyeviti wa vijiji tunao ambao ndio wanafanya kazi kule nikapendekeza kwamba Madiwani tuwapeleke Serikali Kuu ili zile fedha zilizokuwa zinalipa Madiwani ziende na zenyewe zikasaidie kuwalipa posho angalau ya shilingi laki moja wenyeviti wetu wa vijiji, na wao waweze kutekeleza majukumu yao na wajibu wao kwa weledi kuliko sasa wanapata posho ya shilingi 10,000 na wakati mwingine hazilipwi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini hilo Mheshimiwa Waziri atakwenda kulichukua kama alivyoelekeza Mama, naamini watamshauri vyema, hali kadhalika na mama aweze kuona kwa jicho la kipekee kwa ajili ya kuwasaidia wenyeviti wetu wa vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende sasa kwenye hotuba ya Waziri na ninaomba nianze na suala zima la kodi ya majengo. Wamesema Wabunge wengi, lakini na mimi naomba niseme hofu yangu kwenye suala zima la kodi ya majengo. Mheshimiwa Waziri anatuambia kwamba itakwenda kulipwa kwa mfumo wa LUKU na kila mwezi italipwa shilingi 1,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi ya majengo kwa kila nyumba ni shilingi 20,000. Ukilipa kila mwezi shilingi 1,000 kwa mwaka mzima utakuwa umelipa shilingi 12,000 hii shilingi 8,000 nani anaifidia? Niombe nisaidiwe ufafanuzi kwenye suala zima hili la kodi ya majengo. Lakini ukiangalia tu kwa uhalisia wa kawaida ni kitu ambacho hakiwezekani, kwamba mpangaji niende nikampe huo mzigo wa kulipa kodi ya jengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwenye kodi ya majengo pia ametuambia kwamba shilingi 1,000 na shilingi 5,000 kwenye nyumba yenye mita moja, na zile nyumba ambazo zina mita zaidi ya moja zinatengenezewa mfumo wao, ni lini zinakwenda kutengenezewa huo mfumo? Imekuaje watengeneze huo mfumo wa kodi ya jengo kwenye nyumba yenye mita moja wakashindwa kutengeneza huo mfumo wa nyumba yenye mita zaidi ya moja? Kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri aende akakae na timu yake vizuri watengeneze namna bora ambayo tunaweza kwenda kukusanya kodi hii ya majengo ili tuweze kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017/2018 nikiwa nachangia bajeti hii nilisema kwamba Serikali imekuwa haipunguzi kodi kwenye vifaa vya ujenzi, lakini inakwenda kuongeza kodi kwenye vifaa vya ujenzi huku wanataka kodi kwenye majengo. Ukiangalia hapa kwenye ongezeko la ushuru wa forodha, Mheshimiwa Waziri amekuja na mapendekezo ya kuongeza ushuru kwenye bidhaa ya mabati asilimia kumi au Dola za Kimarekani 250. Sasa tunataka wananchi wetu waweze kujenga na kuishi kwenye nyumba bora leo unakwenda kuwaongezea kodi huko kwenye hizo bati ni mwananchi gani atakayeweza kwenda kujenga nyumba kwa kwenda kupandisha kodi ya mabati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaturudisha nyuma tena watu hawa watarudi nyuma, hawataweza kwenda kumudu gharama za kununua mabati na matokeo yake nyumba za mabati zitapungua tutakwenda kuanza kurudi kwenye nyumba za matope za full suit juu na chini kama enzi hizo tulizotoka huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalo nimuombe Mheshimiwa Waziri, kama umeamua kuchukua kodi ya majengo tunaomba basi punguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi; na kama mnaamua kuchukua kodi kwenye majengo basi huku kwingine tuache ili watu waweze kupumua na waweze kuona ni namna gani wanaweza kuichangia Serikali yao kwenye suala zima la kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye kuzungumzia suala la barabara zetu za kimkakati za kuunganisha mikoa pamoja na wilaya. Ili tuweze kukuza uchumi wetu; na Tanzania sisi tunategemea sana suala zima, la kilimo na kilimo bila barabara hatuwezi kupata tija kwenye kilimo. Sasa sisi mikoa minne, Mkoa wa Tanga, Manyara, Dodoma na Singida tuna barabara yetu ya kutokea Kilindi. Nilisema, kwamba, barabara hii ina ahadi ya marais watatu, Rais Awamu ya Tatu, Rais Awamu ya Nne na Awamu ya Tano waliahidi kuijenga barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na barabara hii sisi kwenye uchumi ndiyo barabara itakayoweza kusaidia wakulima wetu kuweza kupata tija kwenye mazao yao. Lakini pili, ni juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu amezindua zao la kimkakati kwenye mikoa mitatu, mkoa wa Dodoma, Singida pamoja na Simiyu. Kama barabara hizi hazitakwenda kupitika na hizi ndoto za mazao ya kibiashara ya kimkakati ambayo tunaenda kuyapeleka kwenye maeneo yetu, haya mazao pia itakuja kufikia hatua wananchi wamelima mazao haya lakini watakosa barabara za kuzipitisha mazao haya kwa ajili ya kwenda sokoni na kwenda kwenye viwanda vyetu. kwa hiyo mwisho wa siku hatutakuwa na tija kwenye suala zima la malengo ama na matarajio yetu ya kwenda kupandisha uchumi wa taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeiona barabara hii kwenye mpango, lakini kwenye bajeti mmeweka kujenga barabara kilometa 20. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, kwa umuhimu wa zao la alizeti ambalo tunalima Mkoa wa Dodoma na Singida niombe barabara hii Mheshimiwa Waziri ukaingalie kwa jicho la kipekee iende ikajengwe kwa haraka ili tuweze kupata tija kwenye suala la zao hili la mkakati ambalo Serikali mmeweza kuliona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana tena na suala hilo hilo la ujenzi wa barabara zetu hali kadhalika Serikali imekuwa ikipata kigugumizi sana kwenye suala zima la ulipaji wa fidia. Tunapokwenda kujenga barabara zote na maeneo mengine suala la ulipaji wa fidia Wizara ama Serikali mmekuwa mkipata kigugumizi na kuchelewesha ulipaji wa fidia ambao umetusababishia miradi mingi kushindwa kumalizika kwa wakati na hivyo hasara kwa wakandarasi wetu pamoja na kuchukua muda mrefu kumaliza miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mnapokwenda kutekeleza miradi ya kimikakati niwaombe sana, kwa suala la ulipaji wa fidia, fedha hizo zitoke kwa haraka na hatimaye tuweze kuwa tunakwenda kwa kadri ambavyo tunajipangia sisi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la utekelezaji wa bajeti na nitazisema wizara chache, pia suala zima la utekelezaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo kwenye wizara mbalimbali hali kadhalika Serikali imekuwa na kigugumizi sana. Waziri wa Fedha kwa kweli Wizara yako imekuwa na changamoto kubwa kwa kuwa mmekuwa mkichelewesha kupeleka fedha kwenye wizara zetu. Vilevile hata mkizipeleka pia hamzipeleki kama Bunge lilivyopitisha, mnapeleka kidogo kidogo ambazo mwisho wa siku haziendi kwenda kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo kwa kipindi cha miaka mitano Wizara hii imepelekewa fedha za maendeleo asilimia 19.3, lakini Wizara ya Mifugo kwa miaka mitano pia mfululizo wamepelekewa fedha za maendeleo kwa asilimia 21, yaani hata asilimia 30, 50 haijafika. Kwa hiyo tunaona ni kwa namna gani Wizara ya Fedha mnakwamisha maendeleo ya taifa letu kwa kuvuta miguu kwenda kupeleka fedha kwenye shughuli za maendeleo kwa ajili ya kuweza kuleta tija kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sheria ya Petrol kuongeza tozo ya mafuta ya taa, na Mheshimiwa Waziri pendekezo lake anasema anakwenda kuongeza tozo ya mafuta ya taa ili kudhibiti wafanyabiashara wakubwa wanaokwenda kutumia mafuta ya taa kuchakachua diesel na petrol. Mheshimiwa Waziri yaani umekaa na watalaam wako, mkachakachua, mkapanga, mkapangua mkazichanga karata ukaona mbinu rahisi ama njia rahisi ni kwenda kupandisha mafuta ya taa ambayo ndiyo nishati peke yake iliyobaki kwa wananchi wengi ambao bado hawajafikishiwa umeme vijijini?. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri niombe nenda kwenye suala zima la uongezaji mafuta ya taa hiyo shilingi mia moja uliyoiongeza, hebu nenda kajipangeni upya. Tunafahamu fika, hata wewe Iramba kwako unajua ni vijiji vingapi vyenye umeme? Nenda, watu leo bado wanatumia mafuta ya taa, tunapoendelea kuongeza huu mzigo wa shilingi mia kwa wananchi wetu haikusaidii, hata wewe utakuja kuulizwa ulikuwa na maana gani? tuwaache hawa watu, tafuta namna ya kuwadhibiti hawa wanaochakachua huku, punguza mzigo kwa mtanzania mnyonge asiyekuwa na hatia. Kwa hiyo nenda ukaondoe kodi hii ili wananchi wetu waweze kupata nafuu ya maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la shilingi mia moja pia kwenye lita ya kila mafuta ya petrol na diesel; nimalizie tu. Pia hili nalo nikuombe Mheshimiwa Waziri nenda kaliangalie, ukiongeza tozo tena kwenye petrol na diesel hali kadhalika maisha yatapanda, nauli zitapanda, vyakula vitapanda kwa sababu vinasafirishwa, kwa hiyo gharama ya maisha inakwenda kupanda huo mzigo anaenda kubeba mwananchi wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie la mwisho. Ahadi nyingi za viongozi wetu waliopita zimekuwa zikisemwa humu ndani mara kwa mara na ni wajibu wetu kwa sababu ahadi ni deni; na siku zote ahadi zinazoahidiwa na viongozi wetu kwa mfano Mheshimiwa Rais au Makamu wa Rais ama Waziri Mkuu inakuwa ni taasisi siyo mtu binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mwaka 2015/2020 Serikali Awamu ya Tano iliwaahidi Watanzania kuwapatia milioni 50 kila kijiji, lakini mpaka sasa bado sijawahi kuisikia wala kuiona hii milioni 50. Ahadi ni deni, Mheshimiwa Waziri wa Fedha niombe hii milioni 50, kwa kuwa ni ahadi kama ahadi zingine na wananchi wetu Watanzania waliopo huko bado wana matumaini wanasubiri milioni 50 kila Kijiji, niombe sasa hii milioni 50 kila kijiji itolewe ili wananchi wetu waende wakapate mitaji yenye tija na waweze kujenga uchumi wa taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru na mimi kunipatia nafasi ya kuweza kutoa mchango wangu kuhusiana na suala zima la hizi sheria ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Kamati ya Sheria Ndogo kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwa niaba ya Bunge ama kwa niaba ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria ndogo imetueleza vizuri kwamba lengo la madhumuni ya kuwepo kwa hizi sheria ndogo. Tunapokwenda kutunga sheria kwa mfano sisi Wabunge, sisi Wabunge humu ndani wote si wanasheria, lakini Ofisi ya Spika imeamua kuwa na utaratibu kunapokuwa na Muswada, kunapokuwa na jambo lolote linalohusu sheria Kamati inayohusika either ya sheria inayotungwa kwenye Wizara yoyote ile Kamati kupatiwa fursa ya kupewa uelewa wa pamoja ili Bunge linapokwenda kufanya maamuzi ya sheria husika Wabunge wote waweze kuwa na uelewa wa sheria hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kwenye halmashauri zetu Madiwani wetu ndiyo wanaopitisha ama ndiyo wanaotunga hizi sheria ndogo, lakini Madiwani wetu hawapati fursa ya kupitishwa ili waweze kupata uelewa wa hiyo sheria inayokwenda kutungwa ina madhara gani kwenye halmashauri hiyo, ama ina madhara gani kwa wananchi wa eneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, cha kwanza niiombe Wizara inayohusika na suala zima la halmashauri iweze kuona ni namna gani inakuwa inawapa semina Madiwani wetu ama inawapa elimu elekezi ya kwanza kabla hawajaanza kutunga hiyo sheria ili Madiwani wetu waweze kupata uelewa wa pamoja na wanapokwenda kutunga hiyo sheria iweze kuwasaidia wananchi na si kuwakwaza na kuwakandamiza wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna wanasheria pia wa halmashauri. Wanasheria wetu wa halmashauri pia kutokana na wingi na shughuli nyingi zilizopo ndani ya halmashauri na wao pia wamekuwa nyuma kwenye suala zima la utungaji wa sheria. Lakini pili, wamekuwa hawapati semina ambazo zinawasaidia kuendelea kuwaongezea uwezo ili waweze kulishauri Baraza vizuri na kwenda kutunga hizo sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pia niishauri Serikali kwamba waweze kuona sasa ni wakati umefika wa kuweza kuwapatia semina wanasheria wetu ndani ya halmashauri ili waweze kuendelea kuongeza uwezo na kuweza kuwasaidia Madiwani wetu kwenda kupitisha hizo sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na kanuni nyingi sana ambazo zinatungwa na halmashauri na kanuni hizi zinatofautiana kwa kila halmashauri na kwenye kila halmashauri inategemea Halmashauri za Mijini, Halmashauri za Majiji, Halmashauri za Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye Halmashauri za vijijini; waliopo wengi vijijini ni wakulima na wafugaji. Kwenye halmashauri zetu kuna kanuni ambazo zinatungwa suala zima la ukusanyaji wa mapato ambalo na wewe umetoka kulizungumza asubuhi ya leo. Mkulima amelima hajapewa mbegu na Serikali, hajapewa jembe na Serikali, mvua ya kutegemea Mwenyezi Mungu, hana chochote ambacho amewezeshwa, amelima ndani ya halmashauri yake, anatoa mazao yake shambani mkulima anaenda kukutana na geti limewekwa barabarani eti alipe ushuru wa mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujakataa kuchangia maendeleo ya Taifa letu, lakini je, tunachangia kwa utaratibu upi? Mkulima aliyelima kwa jasho lake anatozwa ushuru anayekuja kununua mazao kwa mkulima anachajiwa ushuru mdogo sana, kwa mfano, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba. Mkulima shambani anatozwa gunia shilingi 1,500 huko mashambani, lakini huyu mnunuzi ambaye amekuja kununua mazao anaambiwa yeye anapewa kibali cha kununua mazao jumla analipa shilingi 750. Sasa hivi vitu sheria zinakuwa kwa namna gani yaani mkulima aliyelima yeye ndiye anayezalisha kwenye eneo husika kanuni zetu ambazo Madiwani wetu huku wanazozitunga zinakwenda kumkandamiza huyu mwananchi wa chini halafu zinam-fever huyu mtu wa juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukija kwenye suala zima la mifugo kwenye halmashauri za vijijini tuna minada ya mifugo, hii minada ya mifugo inamtaka mfugaji anapotaka kwenda kuuza mfugo wake siyo maeneo kata zote zenye minada anapotoka kwenye Kata A kwenda Kata B kuuza mfugo wake ni lazima awe na kibali na kile kibali ni cha kumtambulisha yeye aweze kutambulika kwamba ule mfugo ni wa kwake na anahitaji kwenda kuuza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye halmashauri zetu wametunga sheria ya hizo kanuni za kum-charge mfugaji fedha ya kupeleka ng’ombe wake ama kuku wake ama mbuzi wake kwenda kuuza mnadani, halafu yule anayenunua kule hawam-charge, mfugaji yeye anakuwa charged, lakini mnunuzi akinunua yule ng’ombe anachukua ile risiti ya mfugaji ndiyo anatembea nayo barabarani na kwenye magari mpaka anafika anakowapeleka. Kwa hiyo, ukiangalia hizi sheria bado Madiwani wetu hawajawa na uelewa mzuri wa namna bora ya kuweza kutunga hizo sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna kanuni pia za Mawaziri, naomba nizungumzie Wizara ya Afya ni kweli kwamba wakina mama wajawazito wanatakiwa waweze kufika kliniki lakini pia waweze kujifungulia kwenye kliniki zetu, lakini ni ukweli usiofichika kwamba kwenye maeneo yetu yaliyo mengi bado hatujawa na zahanati za kutosha kwenye maeneo yetu, hatuna vituo vya afya vya kutosha kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mama huyu akitoka zaidi ya kilometa 20 ama 30 kwenda kutafuta hicho kituo cha afya ama zahanati ni mbali, wakati mwingine uchungu unapokuja anakuwa bado hajajiandaa wala hajui ni saa ngapi uchungu utafika, akijifungua anapotoka nyumbani anaenda anampeleka mtoto wake kliniki anapigwa faini na mimi kwangu halmashauri ya Wilaya ya Chemba mwaka 2020 nilikutana na hicho kitu wakati wa kampeni, ilikuwa mtoto mwanamke akijifungua mtoto wa kiume anakuwa- chaeged faini akijifungulia nyumbani akienda kliniki anakuwa charged faini mtoto wa kiume shilingi 30,000, mtoto wa kike shilingi 50,000 wakiuliza hizi ni kanuni tumeletewa, hii ndiyo sheria tunayo tekeleza sisi tumeletewa ili tuweze kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, muone kwamba wakati mwingine hivi vitu either inaweza hata haikupelekwa, lakini kwa kuwa wananchi wetu hawana uelewa wanakwenda kujificha watumishi wetu watekelezaji wa hizi kanuni na sheria wanaenda kuwaumiza wananchi wetu kwenye maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI suala zima la watoto wetu kupata chakula shuleni; hatukatai ni jambo jema sana ili kumpunguzia mtoto umbali ule mrefu wa kwenda na kurudi apate chakula shuleni ili aweze kuendelea na masomo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mzazi ana watoto wanne wako shuleni, shule imeamua kujipangia utaratibu na mbaya zaidi hawashirikishi kabisa wazazi wanakaa Kamati ya Shule kule, inapanga, inaanza kupeleka migambo huko chini kwamba mzazi ana watoto wanne anapangiwa kila mtoto apeleke gunia la mahindi kwa muhula, debe la maharage. Mzazi huyu anakuwa hana uwezo wa kuweza kuwahudumia hawa watoto wote apeleke magunia manne na debe nne za mahindi anaanza kulipa kwa awamu kidogo kidogo let say huyu wa kwanza kamlipia, wa pili hivyo ili aweze kupunguza huo mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kusikitisha wazazi hawa wamekuwa wakifanyiwa vitu vya ajabu, mzazi anaenda anakamatwa na mgambo kwa nini hajalipa chakula cha mtoto, okay akikamatwa na mgambo hela ya mgambo anatakiwa alipe yeye 30,000 anaenda kwenye Baraza la Kata anaambiwa alipe fedha ya Baraza, akitoka hapo anatakiwa kupigwa faini na Kamati ya Shule eti ameshindwa kulipa chakula kwa ajili ya watoto kwenda kupata chakula shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hizi kanuni bado tuone ni kwa namna gani zinakwenda kufanyiwa utafiti ili tuweze kukidhi mahitaji ya wananchi wetu huko chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine hizi kanuni zote na sheria zote zinatungwa ili ziweze kuwasaidia wananchi wetu wasiweze kupotoka kwenye maeneo mbalimbali, lakini zitungwe sheria ambazo ni rafiki na kabla ya kutungwa tuwashirikishe watu husika ambao wanatekeleza hiyo sheria tusitunge sheria halafu mwisho wa siku watekelezaji inakuja kukutana nalo barabarani halafu mwisho wa siku inakuja kutuletea shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni kuhusiana na suala zima pia ya hizi sheria zetu na Kamati pia wamelisema, sheria zinatungwa wakishatunga kabla hazijatangazwa kwenye Gazeti la Serikali sheria zinaanza kutumika matokeo yake zinaleta hasara kubwa sana kwenye halmashauri zetu kwa sababu zikianza kutumika mtu anaamua kwenda kushtaki, akishtaki halmashauri ikipelekwa kule kesi tunaenda tunashindwa kwa sababu sheria kwanza haijatangazwa kwenye Gazeti la Serikali haikuwa tayari kwa matumizi. Kwa hiyo, mwisho wa siku tunaingiza halmashauri kwenye madeni makubwa ya kulipa gharama mbalimbali ambazo hazikuwa na sababu. Kwa hiyo. Mimi niwashauri pia Serikali waweze kuona kuelekeza halmashauri zetu zinapotungwa sheria hizi ndogo ndogo zihakikishwe zinaanza kutumika baada ya kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi siku ya leo niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Afya na ninaomba nianze tu na suala zima la upungufu wa wahudumu wa Wizara ya Afya na naomba nilisemee kwa Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Dodoma ni Mkoa ambao umekwenda sasa kupata ongezeko kubwa sana la wageni kutoka nje na tuna Hospitali ya Rufaa kwa maana ya Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, lakini pia tuna Hospitali ya Benjamin na hospitali zingine za taasisi, lakini kumekuwa na changamoto kubwa sana ya foleni ama msongamano kwenye hospitali hizi. Nilikuwa nataka Mheshimiwa Waziri ukija naomba utuambie wananchi wa Dodoma msongamano huu, mkakati wako ni nini wa kuepusha msongamano kwani watumishi kwa maana wageni wengi ambao wameingia ni watumishi wa Serikali na mara nyingi wanatumia kupata appointment na madaktari wanapofika pale hospitalini hawapangi foleni. Wenyeji wa Mkoa wa Dodoma wanapanga foleni Mheshimiwa Waziri mpaka siku tatu mtu hawezi kumuona daktari, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja uweze kuniambia suala hilo linatatuliwaje kwa udharura wa ongezeko la watu katika Mkoa wetu wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kusemea suala zima ni sera ya Serikali kwamba kila mkoa unatakiwa kuwa na Hospitali ya Mkoa, Wilaya kuwa na Hospitali ya Wilaya, lakini pili kata kuwa na vituo vya afya na vijiji kuwa na zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi wamekuwa wakisimama hapa wanalalamikia suala zima la hospitali za Wilaya na vituo vya afya. Mkoa wangu wa Dodoma una Wilaya saba, Wilaya tatu hatuna hospitali. Tumekuwa tukiomba fedha mara kadha wa kadha na fedha hizo hazitoki. Sasa Mheshimiwa Waziri suala la ongezeko la watu hapa Mkoa wa Dodoma linakwenda pia kuleta changamoto kubwa kwa sababu wananchi wa Wilaya za pembezoni zote wanapokosa huduma huko kwenye Wilaya zao wanakuja hapa Makao Makuu kwa maana ya Hospitali ya Mkoa wa Dodoma. Sasa leo Wilaya hizi hazina hospitali za Wilaya, lakini bado kuna msongamano mkubwa, naomba utuambie Mheshimiwa Waziri hizi Wilaya tatu nini hatma yake kwenye bajeti hii ya fedha ya mwaka huu 2018/2019. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Chemba ina kata 26. Kati ya kata 26 ni kata nne tu ndiyo ina vituo vya afya, lakini tuna kituo cha afya Kituo cha Hamai, kituo hiki nilikisemea Bunge lililopita ama kikao cha bajeti kilichopita. Hiki ndiyo kituo kinachotumika kama Hospitali ya Wilaya ya Chemba, lakini cha kustaajabisha na cha kusikitisha kituo hiki kina watumishi 16, kituo hiki hakina maji, kituo hiki hakina x-ray machine, kituo hiki hakina gari la wagonjwa. Kituo hiki acha tu kwamba kinahudumia kama kinakuwa kina-take charge ile ya wagonjwa wa Wilaya ya Chemba, lakini pia kinahudumia Wilaya ya Kiteto, kinahudumia Wilaya ya Chamwino, kinahudumia Wilaya ya Kondoa. Hivi vitu hebu tunaombeni muwe mnatuona na watu wengine huku, msiwe mnagawana gawana tu hizi fedha halafu watu wengine mnatusahau. Mngeacha hata kutujengea ule uwanja wa Chato kwa shilingi bilioni 42 mkatuletea hizi fedha zingeweza kutusaidia kujenga hizi hospitali zetu za Wilaya ikaweza kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hii shilingi trilioni 1.5 ambayo inapigwa pigwa chenga na Serikali mimi naamini ipo mahali, mlikuwa mnatikisa kiberiti, sasa tunaomba muitoe hadharini ije iende ikatekeleze shughuli za maendeleo kwa kutoa huduma ya afya, kwani tunaamini Mama Salma amesema kwamba bila afya hakuna uchumi. Mnatangaza Serikali ya viwanda, Serikali ya viwanda Watanzania wagonjwa hawana dawa, hakuna wahudumu, Tanzania ya viwanda iko wapi?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninaomba sana kwa jinsi mnavyojinasibu Serikali sikivu tunaomba usikivu huo uende kwenye shilingi trilioni 1.5 ikatuletee madawa na kulipa mishahara ya watumishi katika Taifa letu ili Watanzania waweze kwenda kuendelea.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niseme kwamba hakuna Mbunge hata mmoja ambaye anaamini kwamba maji siyo muhimu. Nisikitike tu watu wanaopinga suala zima la kuundwa kwa tume ya kwenda kuchunguza hali halisi ya miradi ya maji kwenye maeneo yetu. Leo kama Wabunge tungekosa maji hakuna Mbunge hata mmoja angekuja humu ndani, hayupo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uundwaji wa tume, Wabunge tunahitaji tume iundwe kwa sababu tumekuwa tukizungumza suala zima la ufisadi kwenye miradi ya maji, Serikali kwa maana ya Wizara mmekuwa hamtuelewi. Mwaka jana nilizungumza suala la Mradi wa Ntomoko, mwaka juzi hali kadhalika, mradi huu sikuwahi kupata majibu, uliendelea kupigwa danadana kwenye vitabu vya Waziri, safari hii hata kwenye kitabu cha Waziri Mradi wa Ntomoko haupo na matokeo ni mpaka Rais ndiyo amekwenda kutoa kauli ya kwamba waliotumia fedha za Mradi wa Maji Ntomoko wachukuliwe hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tuna kosa gani Wabunge tukisema Mawaziri hawako tayari kwenda kufanya kazi na kusimamia miradi hii ya maji kwa ukamilifu wake? Kwa nini tukisema kwamba Mawaziri mmeshindwa, amebaki mtu mmoja peke yake ndiye anayetoa kauli za miradi na shughuli mbalimbali za Serikali kutendeka.

Suala la Ntomoko tumelisema hapa miaka nenda, miaka rudi, hamkuwahi kusema chochote na hamjawahi kuchukua hata hatua yoyote mpaka Rais amekwenda kuchukua hatua. Sasa ninyi Mawaziri kazi yenu ni nini, si bora mtoke wote abaki Rais Magufuli peke yake afanye kila kitu, ninyi mnafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la upatikanaji wa maji nchini ni changamoto kubwa sana. Vijijini kuna shida ya maji wote humu ndani sisi ni mashahidi. Taabu hii wanaoipata ni wanawake wanaoishi vijijini. Mwanamke wa kijijini kulala kwake analala saa mbili, anaamka saa saba za usiku, saa tisa za usiku anatembea zaidi ya kilometa 20, 40 anakwenda kutafuta maji, anarudi mwanamke huyu amechoka bado anatakiwa kwenda kuihudumia familia yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini watoto wetu wa kike wanapata taabu kubwa sana. Leo watoto wa kike wanapata mimba za utotoni kwa sababu ya kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kwenda kutafuta maji na Serikali mnawakatalia watoto wetu wa kike kurudi shule wanapopata mimba za utotoni eti kwa sababu amepata mimba, akienda shuleni atakuwa ni mzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Chama cha Mapinduzi haina dhamira ya dhati ya kwenda kumtua mwanamke na mtoto wa kike ndoo kichwani. Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaendelea kumdidimiza Mtanzania wa chini aendelee kudidimia kwenye shughuli za kiuchumi, elimu na hatimaye sisi Wabunge tulio wengi wa Chama cha Mapinduzi tunaopata maji safi na salama, elimu bora na familia zetu zinasoma vizuri ili watu hawa wanyonge wa huko chini watoto wao wasisome, wasipate maji safi na salama, wafe kwa maradhi, ili familia zenu viongozi wa Chama cha Mapinduzi waje waendelee kuliongoza Taifa hili. Dhambi hii Mwenyezi Mungu anawaona na hakuna malipo yanayokwenda kulipwa akhera, tutalipana hapahapa duniani na kila mmoja ataonja jasho lake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala zima la madeni ya taasisi za maji. Mwaka jana nilisema taasisi za Serikali zinadaiwa na Mamlaka za Maji zikiwemo Ofisi ya Rais, Ofisi ya Makamu wa Rais, JKT, Polisi na Magereza. Taasisi zote hizi za Serikali zinadaiwa na Mamlaka za Maji. Kibaya zaidi unakuta taasisi hizi zinadaiwa hazikatiwi maji, Mtanzania/ mwananchi wa kawaida anadaiwa mwezi mmoja tu hajalipa anakwenda kukatiwa maji, huu ni uonevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mbaya zaidi Jeshi la Polisi kwa hapa Dodoma ilifanyika operesheni, walivyokwenda kukatiwa maji Jeshi la Polisi likaamua kukamata magari yote ya DUWASA pamoja na pikipiki, vifaa vyote vikakamatwa vikaenda kujazwa pale kwenye kituo cha polisi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi. Mimi naamini kuwa kila mtu anapofanya kazi anatakiwa anapopata ujira wake autumie bila ya mtu yeyote kumuingilia katika kipato chake. Wafanyakazi wa nchi hii wanafanya kazi na wanalipwa mshahara hakuna Serikali yoyote ya nchi hii inayokwenda kumpangia matumizi mfanyakazi yule ya mshahara wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini wakulima wanalima kwa shida, kwa taabu wanapovuna mazao yao mnataka kuwapangia namna ya kuyatumia mazao yao? Nimwombe Mheshimiwa Waziri akija hapa, pamoja na kwamba zigo hili tunamtwisha lakini yeye ndiye mwenye dhamana na Wizara hii, aje atuambie hivi ni kwa nini wakulima hawa ambao hamuwapi mbegu, wananunua mbegu kwa shida ambazo bei zake ni aghali, pembejeo mnachelewesha na wengine kwa mfano huku Dodoma sisi pembejeo za Serikali hatuzijui kabisa, hamuwasaidii kitu
chochote kile lakini mnataka kuwapangia namna ya kutumia mazao yao pale wanapokuwa wamevuna? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala zima la mbegu za mahindi; kilo mbili ya mbegu ya mahindi inauzwa shilingi 14,000. Mwananchi huyu anapanda mbegu ile ya kilo mbili kwa shilingi 14,000, leo ndani ya Mkoa wa Dodoma, Wilayani kwangu Chemba wakulima wale wanauza debe la mahindi shilingi 2,500. Mbegu kanunua kilo mbili Sh.14,000 lakini debe la mahindi anauza shilingi 2,500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wakulima tunachowataka ni nini? Yaani hii shilingi 2,500 anayouza hata nusu kilo ya dagaa hana uwezo wa kununua ili aweze kula. Mtu huyu anatakiwa kuuza madebe mawili apate shilingi 5,000 aende akanunue kilo moja ya sukari aweze kunywa chai ama uji na familia yake. Hiki kitu hakikubaliki na Mheshimiwa Waziri ukija mimi nitaomba unisaidie tu, umejipangaje na Wizara yako kuhusiana na upatikanaji wa mbegu ambazo zitapatikana kwa urahisi na kwa gharama ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la pili kuhusiana na migogoro ya ardhi. Tumeona migogoro mingi ya ardhi inayotatuliwa leo ni upande wa maliasili tu. Wakulima hawa pamoja na shida kubwa wanayoipata ya kulima chakula na sisi Wabunge tunakula chakula cha wakulima hao lakini mahali pa kulima nako pia imekuwa ni changamoto. Migogoro ya wakulima watu hao wanakufa kifo huku wakiwa wanajiona wao wenyewe wanakufa na kitanzi chao. Hawana watu wa kuwapigia kelele kwenye migogoro na wakisema wanaonekana ni wakorofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mheshimiwa Waziri akija aniambie suala la migogoro ya ardhi ya wakulima nini mkakati wake kwenye bajeti hii ya fedha ya 2018/2019 ili wananchi wetu wakulima hawa ambao wanafanya kazi kubwa ya kutafuta chakula kwa ajili ya Taifa letu tuweze kuona namna gani migogoro hiyo inakwenda kutatulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akija naomba wakulima wangu wa Wilaya ya Chemba, eneo la Sekii pamoja na Champanda nataka aje aniambie mgogoro huu baina ya WMA ya Makame (Kiteto) na wananchi hawa kwenye vijiji hivi hatma yao ni nini? Wananchi hawa wameendelea kunyanyasika, mashamba yale ni ya kwao, Makame WMA wameenda kurudisha mpaka nyuma, matokeo yake watu wetu wanaenda kufyekewa mazao, si sawa sana. Mheshimiwa Waziri akija naomba anisaidie huu mgogoro unakwenda kuishaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala zima la madeni ya mbolea, wameongea Wabunge wengi. Siku za nyuma huko mwaka 2014 na kurudi nyuma, watu hawa pamoja na kuwa walikuwa wanafuja hizo nyaraka na kadhalika lakini walikuwa wanalipwa. Leo ni mwaka wa nne watu hawa hawajalipwa mnadai kwamba mnafanya uhakiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 mlituambia mnahakiki, mwaka 2017 mnahakiki, leo mnafanya nini? Mtaendelea kuhakiki mpaka lini? Hivi kwa Serikali na vyombo vyake vyote mlivyonavyo mmeshindwa kubaini nani anastahili kulipwa na nani hastahili kulipwa? Mheshimiwa Waziri akija tunaomba... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kwa kunipatia nafasi niweze kusema machache kwenye Wizara yetu hii ambayo imebeba Watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaomba nizungumzie suala zima la wagani (maafisa mifugo), lakini pili migogoro na tatu ni ushuru kwenye minada yetu na ntagusia kidogo suala zima la nyavu haramu.

Mheshimiwa Spika, wafugaji wetu wengi walioko vijijini wana changamoto kubwa sana ya wagani ama maafisa mifugo. Kwanza maafisa mifugo hawajitoshelezi, lakini pili hao waliopo hawafanyi kazi ipasavyo kwa mujibu wa maadili yao ya kazi. Leo afisa ugani aliyeko kijijini yeye amekuwa ni mchuuzi. Analipwa mshahara na Serikali lakini bado anapohitajika kwenda kutimiza wajibu na majukumu yake mtu huyu ukimfuata atakwambia kwanzasina usafiri, hilo ni kweli hawana usafiri, lakini pili, akienda kufanya hiyo kazi atakwambia sasa unanipa shilingi ngapi; mtumishi huyu analipwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa watu, maafisa ugani waliopo tunaomba Wizara iweze kuwafuatilia mmoja baada ya mwingine kwa sababu wamekuwa ni kero na changamoto inayosababisha wakulima ama wafugaji wetu kuacha kuwatumia kutokana na biashara yao ya kutoa huduma, badala ya kutoa huduma kwa jamii, wanalipwa mishahara na kodi hizohizo za Watanzania, wanaacha kufanya hiyo kazi wanataka walipwe fedha nyingine ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maafisa ugani hawa bado wana shida ya vitendeakazi. Afisa ugani huyu uliyempeleka kwenye kata pale ana vijiji vitatu ama vinne; kutoka makao makuu ya kata mpaka kwenda Kijiji A unaweza ukakuta kuna kilometa 20 mpaka 30; vijiji vyetu hata vya Mkoa wa Dodoma unavijua jinsi vilivyo; mtu huyu hana usafiri, hana pikipiki wala baiskele. Hivi Serikali hii ya uchumi wa kati, Serikali ya viwanda tunaifikiaje hiyo ndoto bila kuwaboreshea maisha vitendeakazi vya hawa maafisa ugani wetu ili waweze kufikisha huduma kwa wakulima wetu?

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la migogoro ya ardhi; limesemwa na Wabunge wengi lakini suala hili ni kama vile limetulia kidogo, limepoa, lakini linafanyika chini kwa chini, kuna mambo yanayoendelea huko huwezi kuamini. Naibu Waziri alifika Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa, kwenye Pori la Swagaswaga pamoja na Mkungunero. Kuna watu walikamatiwa ng’ombe wao wakiwa wanachunga, si kwenye hifadhi, ni mpakani na hifadhi, wale watu wa hifadhi wakaenda wakawasukumia wale ng’ombe kwenye hifadhi wakawakamata.

Mheshimiwa Spika, walivyowakata wakaenda wakawaambia kila ng’ombe mmoja alipiwe shilingi laki moja. Watu wale wakasema hizo hela kwa sasa hatuna, wakawaambia nendeni mkatafute mrudi. Walivyorudi wakahojiwa kila mfugaji mmoja wewe ulikuwa na ng’ombe wangapi, mfugaji anasema nilikuwa na ng’ombe 200 anaambiwa ng’ombe hawa 200 mara 1000 tujumlishe. Lakini watu hawa walikuwa wakilipa hizo faini, wanapokabidhiwa ng’ombe hawafiki ng’ombe 200, mtu atapewa ng’ombe 150, atapewa ng’ombe 80. Wakiuliza ng’ombe wetu wengine wako wapi wanaambiwa ng’ombe wamepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo haya yanasononesha, mambo haya yanasikitisha, mambo haya yanahuzunisha na yanatia simanzi sana ndani ya taifa letu la Tanzania. Taifa hili, wakulima hawa, wafugaji hawa, huyu mfugaji anatakiwa alipe ada ya mwanafunzi, anatakiwa ale, anatakiwa afanye mahitaji yake yote kulingana na hawa ng’ombe wake. Umeenda umemchukulia ng’ombe wale, umemlipisha faini, unamtaka nini huyu mfugaji? Tanzania ya wanyonge ipi katika taifa letu leo la Serikali ya Awamu ya Tano? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua zinazochukuliwa na Wizara bado hazina dhamira ya dhati ya kwenda kupambana na watu hawa ambao wameendelea kuwadhalilisha Watanzania walio wengi katika taifa hili ambao ndio walipa kodi na wao ndio wanalipwa mishahara na haohao walipakodi wanaowanyanyasa. Naomba watu wale ambao ng’ombe wao hawakurudishwa, Mheshimiwa Waziri ukija naomba uniambie watu wa Mkungunero na Swagaswaga waliokuwa wamekamatiwa ng’ombe wao, hawakurudi, naomba uniambie watu wale mnawachukulia hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Suala Zima la Ushuru wa Minada. Tunafahamu minada haipo kwenye vijiji vyote wala kwenye kata zote, tuna minada ambayo tumeiteua. Lakini ni kwamba katika minada hii, kumekuwa na ushuru wa usafirishaji na kwenda kuuza, mfano mwananchi anayetoka Kijiji cha Mlongia kwenda kuuza ng’ombe Mnada wa Soya, huyu mtu anatakiwa kukata ushuru…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kuniti, nakushukuru.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kwa kunipatia fursa ya kuweza ushauri wangu katika hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyeweza kutujaalia uhai na afya njema imetusababisha tunaendelea kukutana katika ukumbi huu.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nisemee suala zima la huduma ya afya kwa Watanzania. Mheshimiwa Rais amesema kwenye hotuba yake kwamba tumeongeza vituo vya afya, zahanati pamoja na hospitali za wilaya na mikoa na ukarabati wa hospitali zetu za kanda. Kwenye hili, kujenga vituo vya afya kwa maana ya majengo, kujenga zahanati kwa maana ya majengo, kujenga hospitali za wilaya kwa maana ya majengo bila kuwa na dawa pamoja na vifaatiba na wahudumu kwenye hospitali zetu ni sawasawa na kutwanga maji kwenye kinu, mshahara wake ni kuloa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kama jinsi mlivyojenga haya majengo tunwaomba muende mkawaajiri watumishi wa Wizara ya Afya ili waende kwenye hospitali zetu hizo kuanzia zahanati mpaka hospitali zetu za rufaa waweze kupata huduma.

Pili, muende mkanunue vifaatiba. Asubuhi dada yangu Mheshimiwa Ritta aliuza swali kuhusiana na CT-Scan kwenye hospitali ya Mkoa wa Iringa. Lakini hata sisi Dodoma hapa, CT–Scan tunayo Ntyuka pale ni shilingi 200,000; ni Mtanzania gani anayeweza kumudu kipimo hicho? Kwa hiyo niombe Wizara na Serikali iweze kuona kwenda kununua vifaatiba hivi ili Watanzania wenzetu waendelee kupata huduma iliyo bora ya afya na waimarishe afya zao ili waweze kujenga uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala zima la maji; mwaka 2015 mlituahidi wakati wa kampeni mkatuambia mnakwenda kumtua mwanamke ndoo ya maji kichwani. Watanzania tukaenda tukapiga kura, ndoo ya mwanamke kichwani bado haijatulika kichwani. Bado mwanamke wa Kitanzania hususan anayeishi vijijini anateseka kutembea umbali mrefu akiwa na ndoo yake na mtoto mgongoni anatafuta maji.

Niiombe Serikali safari hii mkija kwenye suala zima la Wizara ya Maji, twendeni tukatenge bajeti ambayo haitakuwa bajeti ya maandishi na maneno na ya kusifiana humu ndani, twendeni tukatenge bajeti itakayokwenda kutekeleza miradi ya maendeleo kama jinsi Mheshimiwa Spika tulivyokwenda kuwekeza kwenye miradi mikubwa Stiegler’s, tumenunua ndege. Basi vivyo hivyo hebu twende tukaone suala zima la upatikanaji wa maji ndani ya Taifa letu ili tuweze kuepuka maradhi, lakini pili tupate fursa ya kupoteza na kuokoa muda ambao tunautumia kwenda kutafuta maji. Muda ule utusaidie kujenga uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waswahili wanasema kitanda usichokilalia huwezi kuwajua kunguni wake. Tunapoomba suala zima la Katiba Mpya, sio kwamba tunaomba ili tuweze kujifurahisha. Tumekuwa hatuna imani na suala zima la Tume yetu ya Uchaguzi na unaweza ukasema Kunti unasema huna imani na Tume ya Uchaguzi mbona wewe uko humu ndani, mimi nilishiriki uchaguzi wa Jimbo yaliyotokea ni mengi. Kwa maoni yetu tunatamani hiyo Katiba Mpya ambayo yale maoni ya wananchi waliyoyatoa kwenye mapendekezo ya hiyo Katiba Mpya ambayo yatakwenda kutupatia Tume Huru ya Uchaguzi yanaweza kutujengea faraja sisi wa vyama vya upinzani pamoja na Watanzania kwenda kuamini tena kwamba tutakuwa kwenye Taifa letu uchaguzi wa huru na wa haki na wa kidemokrasia katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi kwa dakika hizo tano naomba niseme ya kwangu machache ambayo nitaweza kuyasema. Zaidi ya watanzania 75% wamejiajiri kwenye sekta ya kilimo. Lakini sekta hii ya kilimo ambayo ndiyo imeajiri watanzania walio wengi lakini ndiyo inayochangia uchumi wa pato la Taifa hili, lakini ndilo linalosababisha sisi watanzania tuendelee kuishi, Serikali imekuwa haitoi kipaumbele kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema wenzangu waliotangulia kwenye suala zima la masoko naomba nizungumzie suala zima la upatikanaji wa pembejeo na suala zima la wagani kwenye sekta hii ya kilimo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha sasa alikuwa Waziri wa Kilimo kwenye Serikali ya Awamu ya Tano na alivyokuja akiwa Waziri wa Kilimo aliwatangazia watanzania kuhusiana na suala zima la upatikanaji wa pembejeo na hususan kwenye suala la mbolea akasema mbolea itakuwa kama Coca Cola. Sasa Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu umerudi huko huko jikoni nikuombe sana suala lile la pembejeo kwenye suala zima la mbolea ile Coca Cola ile tunaitaka safari hii kwenye bajeti hii tuone mbolea inapatikana kwa wakati na yenye tija kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye suala la pembejeo matrekta power tiller na vitu mbalimbali ambavyo vinakwenda kumsaidia mkulima huyu wa chini vimekuwa vikipatikana kwa shida sana. Hata hiyo mikopo ya matrekta imekuwa ni changamoto pia watu wanazungushwa kwelikweli lakini ili uweze kupata hata hilo trekta unatakiwa kuwa na hati. Wizara ya Ardhi nayo imekuwa ni changamoto hata kuwapatia tu zile ardhi za kimila wakulima wetu ili waweze kupata hati hizo waweze kwenda kukopa hayo matrekta.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kujiuliza Serikali ni moja hivi wanashindwaje kuwaamini hawa watanzania kwamba mtu huyu anajulikana anaishi Kijiji fulani ana ekari kadhaa mwenyekiti wa Kijiji yuko pale anamtambua ni kwanini Serikali imekuwa na kigugumizi kuhusiana na suala zima la utoaji wa mikopo ya pembejeo kwa wakulima wetu wadogo huko vijijini na badala yake tumeendelea kuwaacha wanateseka tuna Benki ya Kilimo ambayo inatakiwa kuwasaidia wakulima wa nchi hii haifanyi chochote hakuna mkulima mdogo hata mmoja anaekopeshwa na Benki ya Kilimo tunaambiwa ni Benki ya Kilimo kwenye makaratasi na majina. Ili tuweze kuleta tija kwenye benki hii niombe benki ya kilimo tuirudishe Wizara ya Kilimo ili iweze kuwahudumia wakulima wetu kule chini na hatimae waweze kunufaika na kodi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisemee suala na wagani, bado watanzania tunalima kilimo cha kujisukuma tu cha jana cha leo tunakwenda nacho hivyo hivyo. Wagani ndani ya nchi yetu pia kwenye sekta ya kilimo ni changamoto Wizara inayohusika na kuajiri Wizara ya Utumishi tunaombeni mtuambie shida ni nini inayosababisha kushindwa kuajiri wagani wakutosha kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wagani ni muhimu sana, tunaona hata watu wamoja moja ambao wanajitutumia wenyewe kwa jitihada zao kuweza kulima kilimo cha kuondokana na umasikini, kilimo cha kutoka kwenye mvua ya Mwenyezi Mungu kwenda kwenye kilimo cha kisasa cha umwagiliaji bado wamekuwa wakikosa huduma hii ya ugani kwasababu tu ya Serikali kushindwa kuajiri wagani kwenye maeneo yetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niliombe pia kama kweli tunahitaji tija kwenye sekta ya kilimo na tuweze kujenga na kuimarisha uchumi wa Taifa letu tuhakikishe kwenye bajeti hii inayokuja kwenye sekta ya kilimo twendeni tukaajiri wagani wa kilimo ili wakulima wetu waweze kupata hiyo huduma muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye suala la wagani suala la wagani wako TAMISEMI kwenye kilimo huku hawapo kwa hiyo, pale wanapokwenda kupata changamoto wagani hawa wanashindwa namna ya kuzifikisha mahali husika. Lakini mgani huyu unakuta mgani huyo ni mtendaji wa kata, mgani huyo ni Afisa Mifugo, mgani huyo huyo ndiyo hata yeye anashughulika na masuala ya kilimo kwa hiyo, unamkuta mtu mmoja ana majukumu kadhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba pia kwenye suala zima la wagani wanaohusiana na kilimo tuwarudishe Wizara ya Kilimo ili waende wakasimamiwe na Wizara yao na waweze kufuatiliwa na tuweze kupata tija kwenye suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nigusie kidogo kwa dakika chache zilizobaki miundombinu tunafahamu vizuri nimalizie tu kidogo dakika moja tunafahamu tuna barabara za kimkakati…

NAIBU SPIKA: Nina orodha ndefu hapa Mheshimiwa.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja tu my dear kidogo tu dakika moja ningekuwa nimeshamaliza tuna barabara za kimkakati tangu Bunge la 10 tuliahidiwa barabara ya kutoka Kilindi kupita Chemba tunaenda kuungana na Singida barabara ile mpaka leo bado hatujaweza kuona nini mkakati wake. Niombe Wizara mtakapokuja kuja kuhitimisha tunaombeni tuione barabara ya kutoka Kilindi inayokwenda kupita Jimboni kwangu Chemba…

NAIBU SPIKA: Haya ahsante Mheshimiwa hiyo barabara umeshaitaja, kwa hiyo imeshasikika.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: …nakwenda kuunganisha na Mkoa wa Singida nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa mchango wangu kwenye taarifa hizi tatu ambazo zimewasilishwa na Wenyeviti wetu wa Kamati.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema kwamba, hivi vitu wakati mwingine vinalitia simamzi sana Taifa letu. Mambo haya ya ubadhirifu ambayo yanaendelea kwenye Taifa letu ni kitu cha ajabu sana na kinakwenda kutukatisha tamaa Watanzania hata kwenda kufanya shughuli mbalimbali za kimaendeleo huko chini.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa kawaida kule chini, akiiba kuku anakamatwa, anapelekwa Mahakamani, anasomewa shtaka, anahukumiwa. Leo Mtanzania aliyesoma kwa kodi za akina mama kule chini; wapika pombe, wakulima wanahangaika kutafuta mbolea kwa shida, kasomeshwa na kodi hizo, amepata nafasi ya kulitumikia Taifalake, anaenda kuweka ubinafsi wa hali ya juu kwa kuweka fedha zote kwenye mfuko wake na tumbo lake, na bado sisi kama Taifa tunamwangalia, hatujitendei haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaomba nizungumzie mchango wangu kwenye suala zima la tozo zinazotozwa kwa ucheleweshaji wa malipo ya Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya Serikali. Tunafahamu fika kwamba Serikali huwa inaandaa bajeti; wataalam wetu huko wanatuandalia bajeti, wanatuletea ndani ya Bunge ili tuweze kuijadili bajeti na tuweze kuona kwamba, kutokana na mradi fulani bajeti tuliyoletewa inakidhi mahitaji? Kama haikidhi tuishauri Serikali kuongeza ama kama inakidhi na kubaki, tushaurI Serikali na kupunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachonishangaza, kama Serikali huwa inaleta bajeti, tunajadili hapa, nao wanatuhakikishia kwamba itakwenda kukidhi mahitaji ya kukamilisha mradi, badala yake mradi ule haukamiliki. Mbaya zaidi, miradi hiyo, wao ndio wanaoenda kuingia mikataba na Wakandarasi. Kwenye mikataba hiyo kuna kipengele ambacho kinasema, ukichelewa kumlipa Mkandarasi utatakiwa kumlipa faini ya kumcheleweshea fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha kwenye miradi mbalimbali imeendelea kucheleweshwa kutolewa kwa Wakandarasi wetu wanaotekeleza miradi mbalimbali. Nitasema baadhi ya miradi hapa. Inapocheleweshwa, tukitozwa zile tozo tunakimbilia kwenda kulipa zile faini, tunaacha kwenda kuhangaika kupeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi hapa tukisema kuna dili linalochezwa baina ya mlipaji na mlipwaji tutakuwa tunakosea? Miradi haipelekewi fedha, haikamili, tunaletewa tozo ya kulipa kwa ajili ya ucheleweshaji wa malipo, tunakimbiila kwenda kulipa hiyo tozo. Kwangu binafsi naona kwamba kuna mchezo ambao tunachezewa na wataalamu wetu ndani ya Serikali wa kuchelewesha kwa makusudi kabisa; kwa sababu sisi kama Bunge, bajeti tunakuwa tumeshawapitishia. Kwa hiyo wanafanya makusudi wasipeleke zile pesa za utekelezaji wa miradi ili waweze kupata channel ya kwenda kupiga fedha kwenye tozo kule.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mifano michache kwenye suala zima la ucheleweshaji wa ulipaji wa Wakandarasi, tozo ambazo tumetozwa. Daraja la Kigongo - Busisi kwa taarifa ya CAG tumetozwa faini ya Shilingi bilioni 1.5 kwa kuchelewesha kumlipa Mkandarasi. SGR halikadhalika, tumetozwa faini ya Shilingi bilioni 8.9. Yaani hizi tozo zote tunatozwa. Sisi tunahangaika huku hatuna mbolea; hatuna watumishi maana hatuwezi kuwalipa mishahara, tumeshindwa kuajiri; hatuna maji leo, tunashindwa kuchimba visima, hata kuleta maji kutoka Ziwa Victoria tu yafike hapa Dodoma; watu tunakuwa na foleni ya migao ya maji, lakini kuna watu, washikaji wako hapa wanapiga hela, wamekaa kimya na tunawaangalia, wala hatuna shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kwenye upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, kwa kuchelewesha tu kuwalipa fidia wananchi waliokuwa wanapisha ule mradi, zaidi ya kaya 1,125 tumelipa zaidi ya Shilingi bilioni 22 kwa Mkandarasi. Hivi vitu ni kwa nini nchi hii? Ni kwa nini Tanzania yetu hii? Halafu tunatoka tunaenda kuhangaika nje huko, wakati tuna hela ziko hapa, watu wanazichezea pasipo kuwa na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija Mamlaka ya Ndege halikadhalika tumepigwa faini ya Shilingi bilioni 11.3. Hizi fedha ukizijumlisha hapa nyingi ambazo zingetusaidia kama Taifa kuondoa changamoto mbalimbali tulizonazo ndani ya Taifa letu na tukaishi maisha ya kutokwenda kuhangaika barabarani huko kuombaomba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali na Mawaziri wanaosimamia baadhi ya Sekta. Mwaka 2021 tulipitisha tozo, Watanzania wakati wanalalamika kuhusiana na suala la tozo kuna watu walijitokeza wakasema kama hawawezi kulipa hizo tozo, wahamie Burundi, sijui wahamie wapi? Ila kuna watu wako humu wanapiga hizi fedha, hatushughuliki nao, wala hatuwajibu majibu ya namna hiyo. Hivi nikisema kwamba tunakula nao, nitakuwa na shida gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mtanzania wa chini kule anajihangaikia mwenyewe, tunahangaika naye, tunamkamua mpaka dakika ya mwisho, mpaka tone lake la mwisho la damu, halafu kuna watu fulani tu hapa wapo, wala hawana shida, wanakula bata, wanaendesha magari mazuri wakati kuna mama zetu huko vijijini wanatembea kwa miguu zaidi ya kilometa 20 mpaka 30 kwenda kutafuta maji. Watoto wetu wa kike leo kwa kushindwa kuwasogezea shule karibu, wanatembea umbali mrefu kwenda kutafuta shule, wanabakwa, wanapata mimba za utotoni, wanapata maradhi, tuko hapa, watu wanapiga hela, tunawapigia makofi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Bunge hili leo likafanye maamuzi yatakayoleta maslahi mapana ndani ya Taifa letu kwa kuokoa fedha zinazokwenda kuteketea kwenye maeneo ambayo hayana sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie pia suala la fedha za maendeleo, asilimia 40 kwa halmashauri ambazo zina mapato ya chini na asilimia 60 kwa halmashauri ambazo zina mapato makubwa. Fedha hizi nazo zimekuwa kizungumkuti. Leo fedha zinazotumika kukamilisha miradi ya maendeleo kwenye majimbo yetu ni fedha ya Mfuko wa Jimbo, fedha ya Mbunge. Lakini fedha ya makusanyo ya ndani kwenye halmashauri, Wakurugenzi wetu wamekuwa hawapeleki kwenda kukamilisha miradi mbalimbali ambayo wananchi wanajitolea kule chini. Hivi vitu navyo siyo vya kuvifumbia macho. Naomba tuchukue hatua stahiki kwa wale watu ambao mapato yao yanawaruhusu kwa mujibu wa sheria kuchukua fedha ya asilimia 40 kwenda kumalizia miradi mbalimbali inayotekelezwa na wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, naomba nilisemee suala la mbolea. Namshukuru Mheshimiwa Waziri ametoa ufafanuzi hapa. Pamoja na ufafanuzi alioutoa Mheshimiwa Waziri kwamba hawawezi kuifikisha mbolea kwa wananchi wetu kule chini, wameiweka hapa mjini; hivi mjini hapa ndiyo kuna wakulima? Jana wakati naangalia taarifa ya habari, kuna mwananchi mmoja Songea amefariki akiwa kwenye foleni anasubiri mbolea. Kapanga foleni, ameanguka chini, amekufa pale kutokana na msongamano wa kwenda kutafuta mbolea. Ametoka huko kijijini kwao, ni mbali, amefika pale, foleni ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa tunachomwomba Mheshimiwa Waziri, hao Mawakala wake ambao amewapa hiyo kazi ya kusambaza mbolea, mbolea hii isikae Makao Makuu ya Wilaya ama kwenye hivyo vituo. Tuwapelekee wananchi wetu, tuwasogezee angalau kwenye Makao Makuu ya Kata ambapo kwanza tutapunguza msongamano mkubwa; pili, tutawasaidia wananchi kutembea umbali mdogo kuja kufuata hiyo mbolea kwenye hayo maeneo. (Makofi)

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Hussein Amar.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nimpe taarifa Mheshimiwa Majala. Kufariki kwa yule mwananchi akiwa kwenye foleni akisubiri mbolea, hiyo ni ahadi ya Mwenyezi Mungu, na siyo sababu ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unapokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, namheshimu sana Mzee Hussein, sana, sana. Huyu mtu ingekuwa ni ahadi yake, angefia huko nyumbani kwake. Hata kama alikuwa na maradhi yake, laiti ile foleni isingekuwepo na ule msongamano; na tunafahamu Watanzania wengi kwenye suala la afya pia sio watu ambao tuna utamaduni wa kwenda ku-check afya zetu. Yule mtu hata kama alikuwa na maradhi yake na kwamba ahadi yake imefika, lakini katika yale mazingira, chanzo kilichoripotiwa ni mkulima kufariki kwenye foleni ya kutafuta pembejeo, kwa maana ya mbolea na siyo kitu kingine chochote. Kwa hiyo, kama ilikuwa ni ahadi ama haikuwa ahadi, kafia kwenye foleni ya kutafuta pembejeo. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Kama unamtetea mwanao, well and good, siyo mbaya.

SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, kuna taarifa nyingine kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Godwin Mollel.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nilitaka tu kumpa mwenzangu taarifa. Kwanza nimpongeze kwa mchango wake mzuri wenye input nzuri sana. Ila kwa anachokizungumzia, kwa sababu tunazungumza kwenye Bunge na huwa sababu za vifo haviamuliwi na magazeti, mtu unaweza ukafa ukitembea, unaweza ukafa ukifanya chochote, lakini sababu iliyopelekea kifo ni clinical. Kwa hiyo, namwomba, inawezekana anataka kuonesha uzito wa jambo analolisema, lakini sababu ya kifo haiwezi kuwa kukaa kwenye foleni.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unapokea taarifa hiyo.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, naomba Wabunge, hatuna sababu za kuanza kuvutana, ila mtu amekufa akiwa kwenye foleni ya kusubiri mbolea. (Makofi)

(Hapa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Alisimama)

SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesimama.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kanuni ya 71(1)(a) Wabunge hatupaswi kutoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli.

SPIKA: Mwanasheria Mkuu wa Serikali, taarifa gani haina ukweli? (Kicheko/Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya kifo; kifo cha binadamu huthibitishwa na daktari na vile ville kifo cha mashaka kimetolewa mwongozo kwenye kifungu cha 7 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai. Kwa hiyo, mchango wake inawezekana yeye ana taarifa ambazo ni za upande mmoja, lakini mwenye kuthibitisha cause of death kwa mujibu wa postmortem examination report Kifungu cha 8 huwa inatajwa pale. Kama haijatajwa haiwezi ikawa taarifa ambayo inakuwa classified kuweza kutolewa kwenye mamlaka na kufanyiwa kazi.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, amesimama Mwanasheria Mkuu wa Serikali, akatupeleka kwenye Kanuni ya 71 fasili ya (1) ambayo inazungumzia mambo yasiyoruhusiwa Bungeni. Pia ametupeleka kwenye mchango wa Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala ambapo wakati akichangia alikuwa anaeleza namna ambavyo kuna changamoto kwenye jamii kwa maana ya upatikanaji wa huduma kwa sababu ya taarifa ambazo zipo za CAG na namna ambavyo kuna upotevu wa mapato ambayo yangeweza kusaidia kwenye hayo maeneo mengine. (Makofi)

Sasa hapa jambo ambalo halibishaniwi ni kwamba mtu ni kweli amefariki; na huyo mtu amefariki akiwa kwenye eneo ambalo linatolewa mbolea. Ikiwa hilo siyo linalobishaniwa, kwa sababu mimi katika kusikiliza; maana la sivyo itabidi niitishe Taarifa Rasmi za Bunge; sijasikia kama anasema kilichosababisha kifo ni foleni ya mbolea. Anachoeleza ni eneo alilofia huyo Mtanzania. Ni kwamba eneo alilofia ni eneo la kusubiri mbolea. (Makofi)

Sasa kama kuna taarifa yoyote, pengine kama huyo mtu hajafa, moja; la pili, kama amekufa na hajafia pale ambapo mbolea inatolewa, labda hilo ndilo linaweza kubishaniwa. Ila kwa maana ya kwamba mtu amefariki na amefariki sehemu ambayo mbolea inatolewa, hiyo siyo sababu ya kifo, lakini ni kwamba amefia pale. Eneo ambalo amefia ni la kusubiri mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Kunti Majala, kwa sababu hapa nilikuwa sijaombwa mwongozo, ndiyo maana hamjasikia nikisema mwongozo, lakini ilikuwa inatolewa taarifa ili mchangiaji apokee taarifa vizuri. Kwa hiyo, lazima niliongoze vizuri ili hiyo taarifa iwe imetolewa kwa namna inayostahili. (Makofi)

Kwa hiyo Mheshimiwa Kunti Majala, kwa sababu sijaitisha Taarifa Rasmi za Bunge hapa, mimi ndivyo nilivyosikia. Ila kama umesema kwamba yule mtu amefariki kwa sababu ya kusubiri mbolea, nadhani hata gazeti litakuwa halijaandika sababu ya kifo, ila limeandika eneo ambalo huyo mtu amefia.

Mheshimiwa Kunti Majala, endelea na mchango wako.

MHE. KUNTI MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kutoa huo ufafanuzi vizuri na naamini ulinisikia vizuri na umenielewa vizuri. Wabunge ni lazima tuwe watu ambao tunasikiliza na kutafakari ili tuweze kuchukua maamuzi. Hizi biashara za kuwa tunateteatetea na kujizingazinga na kutaka kufichaficha vitu, unaficha kitu gani wakati kitu kiko hadharani? Ndio maana tunaendelea kuibiwa humu ndani ya Taifa letu kwa sababu ya kubebanabebana kusikokuwa na tija na kuteteanateteana kusikokuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi uliyonipa na naomba niishie hapo kwa mchango maana yake naweza nikaendelea kuharibu hali ya hewa aaidi. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kutoa mchango wangu kwa bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya mwaka 2022/ 2023.

Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na hatimaye leo tumekutana katika ukumbi huu tukizungumza maslahi mapana ya Taifa letu. Kwenye mchango wangu leo naomba kwanza nitajielekeza kwenye migogoro ya ardhi ndani ya Taifa letu. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye hotuba yake. Ukurasa wa 45(75) Ardhi, ametuambia naomba kunukuu: “Ardhi ni rasilimali muhimu katika kukuza uchumi na kuondoa umasikini.” Naomba niishie hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kutambua kwamba ardhi ni rasilimali muhimu, lakini rasilimali hiyo muhimu inaweza ikatuondoa kwenye wimbi kubwa la umaskini wa Watanzania tulionao. Hata hivyo, napata shida kidogo kama Serikali inatambua kwamba ardhi ni rasilimali muhimu na ndio kichocheo cha uchumi katika Taifa letu, ni kwa nini Serikali imekuwa na kigugumizi cha kutatua migogoro ya ardhi ndani ya Taifa letu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imekuwa na migogoro mingi sana ya aina tofauti tofauti. Tumekuwa na migogoro ya mipaka, ya vijiji kwa vijiji, wilaya kwa wilaya, mikoa kwa mikoa, migogoro baina ya hifadhi na wafugaji, wakulima na wafugaji, wakulima na wahifadhi. Migogoro hii tumekuwa tukiisema kila siku. Tangu nimeingia Bunge la 11 nimekuwa nikisema suala zima la migogoro hii. Lakini nakumbuka bajeti ya mwaka 2017/2018 tuliambiwa Wabunge wote, tuainishe migogoro yetu tuliyonayo ndani ya majimbo yetu na ndani ya maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliorodhesha migogoro tukaletewa kitabu kimoja kikubwa sana kila Mbunge akapewa zaidi ya kurasa 1,000, tukijua kwamba Serikali imekwenda kutambua migogoro hiyo na inakwenda kuifanyia kazi. Sio hilo tu, baada ya hilo ikaundwa Tume ya Mawaziri Nane, Bunge lililopita wakatumia helikopta, kodi za Watanzania wakazunguka nchi hii nzima kwenye maeneo mbalimbali kupitia ile ripoti tuliyowapa. Mpaka leo ile ripoti iko chini ya uvungu, haijawahi kutoka hadharani, hivi shida ni nini kwa Serikali Sikivu, inayowapenda Watanzania wake, kwenda kuwaondolea wananchi hawa migogoro ili twende tukakuze uchumi wa Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hicho tu mwaka jana pia Tume hiyo hiyo ya Mawaziri Nane, wamezunguka tena nchi nzima kwenda kukagua migogoro. Walikotoka leo moto umewaka kuliko ilivyokuwa. Watu wanauawa kisa ni mpaka wewe upo Wilaya A na mimi nipo Wilaya B yaani utafikiri sijui tupo Taifa gani hata Ukraine haipo hivyo. Haijafikia namna hiyo katika suala zima la migogoro katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi ina zaidi ya miaka 10, lakini Tume hii hivi inafanya kazi gani? Ukija kwenye bajeti wanapewa mishahara, lakini tunaambiwa Tume hii kazi yake, ni kuratibu na kutoa mafunzo kwa Halmashauri zetu ili Halmashauri ziweze kutekeleza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi ukawa unatengea watu fedha kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kwenda kutatua migogoro, badala ya kwenda kutoa fedha ya kwenda kupima ardhi ya kupanga, kupima na kumilikisha. Leo tunavyozungumza kuna ardhi ya wawekezaji wanatajwa sana. Mkulima leo ardhi yake haijulikani, mfugaji leo ardhi yake haijulikani iko wapi lakini maliasili (wanyama) ardhi yao inajulikana mahali ilipo. Leo mfugaji wa nchi hii mwenye ng’ombe 100, ng’ombe 200 hana tofauti na mtu anayemiliki bangi au madawa ya kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mfugaji wa Taifa letu ambapo pia kwenye hotuba ya Waziri Mkuu amekiri kwamba, tumeongeza pato kwa kusafirisha nyama nje ya nchi, maziwa pamoja na ngozi, lakini ukija kuangalia hali ya mfugaji wa Tanzania malisho anajitafutia mwenyewe, majosho anatafuta mwenyewe, madawa anatafuta mwenyewe, kila kitu anajitafutia mwenyewe. Leo ng’ombe wakitoka wamechunga kwenye Hifadhi, huyo mfugaji hataweza kumiliki chochote kwenye ile mifugo. Tulizungumza Bunge lililopita hata mwaka jana nilisema namna mfugaji wanavyomfanya katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfugaji huyo huyo tukija hata kwenye shughuli zetu mbalimbali hata za Mwenge tu hizi Mheshimiwa Nusrat amesema, mfugaji huyu tunamfuata aweze kutuchangia kitoweo, lakini pili atoe na mchango wa mafuta ili Mwenge uweze kuzunguka ndani ya nchi yetu; na wakati Ole Sendeka anasema suala la Mwenge kwamba ulikuwepo na Mwalimu alisema kwamba utawashwa na nimsaidie tu hiyo nyingine ya kuzunguka ni ya kwake. Mwalimu alisema tutauwasha Mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro na sio kuukimbiza kuzunguka nao barabarani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mifugo ambayo wanachanga vitoweo kwa ajili ya kuzungusha Mwenge barabarani brother pole sana. Ahakikishe apambane apate hati miliki ya kuweza kumiliki ardhi yako ya kuchunga mifugo na ili aweze kupata tija ya mazao yake na mifugo na kujenga uchumi wa familia yake na kipato chake na sio kutetea suala zima la kuzungusha Mwenge, anasema eti ni Mwalimu alisema. (Makofi/Kicheko)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa Taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Kunti kwamba, Mwenge wa Uhuru katika azma yake ya kuanzishwa ilikuwa mwaka 1958 na katika azma ile ile ya yale yaliyoelezwa ni katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na umoja, amani, upendo na mshikamano. Baada ya Uhuru mwaka 1961 tulivyopata Uhuru Mwenge ule uliwekwa Mlima Kilimanjaro na baada ya hapo purpose yake tulipoingia katika Mfumo wa Vyama Vingi vya Siasa ulirithiwa na kuasisiwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa maana ya kwamba ukawa na jukumu sasa la kusimamia masilahi ya nchi. Mojawapo la kwanza, ni kuhakikisha unamulika masuala yote ya rushwa katika miradi ya maendeleo, unakwenda kufanya usimamizi kwa kufanya monitoring na evaluation katika miradi mikubwa ya maendeleo ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zote zinazotolewa katika bajeti ya Serikali hii pamoja na kuwa na Mfumo wa Kiserikali wa kiutawala kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inahitaji kuwa na overseeing body au institution nyingine ambayo inakwenda ikiwa independent kama Mwenge wa Uhuru ambao wajibu wake unapokwenda katika maeneo hayo ni kuhakikisha kwamba, kama kwa mwaka wa jana tu Mwenge wa Uhuru uligundua miradi zaidi ya 46 yenye thamani ya fedha zaidi ya shilingi bilioni 40 na haya mambo yapo kwenye uchunguzi PCCB watachukua hatua. Kwa hiyo, kilichopo kwenye hii dhana… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante amekuelewa. Haya Mheshimiwa Kunti, malizia dakika yako moja.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri alikuwa na muda wa kuja kujibu hoja za Wabunge na huu haukuwa wakati wake. Pili, kwenye suala la ufisadi hiyo hiyo miradi tunayokwenda kuzindua na Mwenge bado tunakutana na ufisadi 150 kidogo. Kwa hiyo, naomba tu Mheshimiwa Waziri atulia muda wake utafika atajibu hoja za Wabunge wala asitake kupata kuwa na haraka. Naomba niendelee na mchango wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la migogoro ya ardhi tuliyonayo leo viongozi wa Chama cha Mapinduzi ambao wamepewa dhamana na Taifa hili; na watu wanaendelea kuumia na kupoteza maisha na mali zao kwa sababu ya kushindwa kufanya maamuzi ya kutatua migogoro kwa kwenda kusema kwamba wewe eneo lako ni hili na wewe eneo lako ni hili. Hawataki kuweka bayana hizo, hakika Mwenyezi Mungu atakuja kuwahesabu siku ya hukumu. Naomba niwashauri kwenye migogoro ya ardhi, cha kwanza Sheria ya Tume ya Mipango ya Ardhi imepitwa na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Sheria hiyo ije hapa tuifanyie marekebisho ili Tume hii tuipe mamlaka ya kuweza kusimamia mpaka chini kwenye halmashauri zetu na kuweza kwenda kutatua hiyo migogoro. La pili, mamlaka zetu za halmashauri ambazo na zenyewe zinahusika kwenye suala zima la upimaji na upangaji na umilikishaji, twende sasa TAMISEMI tunawaomba sasa, waende wakatenge Mafungu kwa ajili ya suala zima la upimaji na umilikishaji wa ardhi kwa wananchi wetu na kwenda kuondoa migogoro. Suala la tatu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuchangia hizi hoja mbili zilizoko mbele yetu, hoja ya Kamati ya Miundombinu pamoja na hoja ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na suala zima la mtiririko wa bajeti kwenye Wizara ya Kilimo na nitaomba nijikite sana kwenye kilimo kwa sababu kilimo zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wanategemea kilimo, kiuchumi na kwenye mambo mengine yote.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana mwezi wa Sita tunaahirisha Bunge hapa, bajeti ambayo ilikuwa ni kipaumbele na tuliyoipigia makofi na kuishangilia ilikuwa ni bajeti ya Kilimo ambayo ilitoka bilioni 200 mpaka tukafika bilioni 900. Tulisema hapa kwamba suala la kutenga hii bajeti liendane na suala zima la kupeleka fedha kwenye Wizara husika ili tuweze kufikia malengo tunayoyakusudia.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa tuna nusu mwaka, Serikali kwa maana ya Wizara ya Fedha wametoa asilimia 19 tu ya bajeti ya maendeleo. Tunavyozungumza hapa, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa dhamira yake njema ya kuwasaidia wakulima na kuinua kipato cha Taifa letu, akaamua kwa kuwa suala la mbolea limekuwa ni changamoto gharama ni kubwa, akaomba Wizara itoe shilingi bilioni 150 ili ziende kwenye mbolea watu wetu waweze kupata mbolea kwa bei ya chini.

Mheshimiwa Spika, leo tunavyozungumza Wizara ya Fedha imetoa bilioni 50, lakini bilioni 50 zenyewe zimetolewa kwa kunatanata hizi, kuanzia mwezi wa Novemba, Disemba na hii Januari ndiyo wanaendelea wamefikisha bilioni 50. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema…

SPIKA: Mheshimiwa Kunti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha amesimama. Mheshimiwa Mwigulu ni taarifa, utaratibu ama?

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika ni taarifa.

SPIKA: Inabidi ukisimama uniambie ili nijue ni Kanuni gani inaniongoza, karibu.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ninampa taarifa mchangiaji Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyoongea hatuna shida ya fedha kwa ajili ya Wizara ya Kilimo, fedha kwa ajili ya Wizara ya Kilimo, kwa ajili ya irrigation, kwa ajili ya mbolea zote zipo hivi tunavyoongea, isipokuwa tunazitoa kufuatana na jinsi certificate zinavyoiva. Mikataba yote ya program imeshasainiwa, kwa hiyo, kadri certificate inavyokuja tunawasilisha na Waziri wa kisekta atasimama hapa akuambie kwamba wanasubiri certificate halafu tulipe, na mikataba yote ilishasainiwa.

Mheshimiwa Spika, inabidi tukubaliane ili tuelewane, fedha hatufanyi kazi ya kugawana tunatekeleza project ndiyo utaratibu wa malipo unavyofanyika. Kwa hiyo, fedha kwa ajili ya irrigation zipo na zinasubiri certificate ili tuweze kulipa, zote zipo hata hela za mbolea zipo.

SPIKA: Haya ahsante sana, Mheshimiwa Kunti unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, naomba nisiipokee na ninaomba niendelee na mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, nimesema hivi, Mheshimiwa Mwigulu unao muda wako pia wa kuja kujieleza haya yote unayotamani kuyaeleza. Fedha bilioni 150 zipo, tunatakiwa tutoe fedha ziende kwa waagizaji wa mbolea ili watu wale waweze kutoa mbolea. Hapa sasa hivi ninavyozungumza magari yapo bandarini yanapakia mbolea, Wahindi wamegoma kutoa magari ya mbolea, vijijini huko hakuna mbolea, msimu wa kupanda Watanzania wamepanda bila mbolea, wamepanda zimeota na mbolea ya kukuzia ni tafrani! Tunakwenda kwenye uzalishaji mbolea ya kuzalisha haipo nchini, sasa yeye ananiambia mbolea ipo unaona raha kuweka hela benki zipo pale zimetulia halafu Watanzania tunapata shida? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizo fedha kama zipo za mbolea bilioni 100 iliyobaki tunaomba kesho ilipwe ili Watanzania waweze kupata mbolea na tuachane na hizi story zenu mnazotuletea.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee na suala la kilimo lakini suala la mbolea zilipwe. Wizara ya Kilimo imesaini mikataba 64 kwenye umwagiliaji, sijui ujenzi wa mabwawa na kadhalika kwenye miradi yao yote. Umesaini mikataba halafu wamekuambia tupe fedha hutoi fedha unatuambia fedha zipo unaziweka hizo fedha zikusaidie nini au zikufanyie nini wewe? Watu wapo tayari kwa ajili ya Kwenda site, mikataba imesainiwa, toeni fedha ili mikataba Wakandarasi waende site wakaanze kufanyakazi za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, tunakuwa tunatarajia kwenye suala la umwagiliaji Taasisi yetu ya ASA inayokwenda kuzalisha mbegu, Wakandarasi hawa walipwe fedha zao ili ASA mwakani tuweze kupata mbegu ya kutosheleza yenye gharama nafuu. Leo tunavyoongea mbegu ya mahindi kilo mbili inauzwa shilingi 14,000 mpaka shilingi 20,000, ukija kwenye mbegu bora ya alizeti inauzwa shilingi 70,000 mpaka shilingi 90,000! Sasa huyu mkulima ni wa namna gani anaenda kupata hizo mbegu kwa namna hiyo?

Mheshimiwa Spika, tulitarajia fedha za umwagiliaji zingetolewa ASA wakapata hizo fedha, mashamba yao yakawekewa mfumo wa umwagiliaji, wakalima mbegu na Watanzania wakapata mbegu kwa gharama nafuu na zinazopatikana kwa wakati, kwa hiyo biashara ya kuambiwa fedha zipo, shida sijui hatugawani hela kama njugu, hiyo miradi mingine mnayogawana kama njugu mbona hatusemi na mnazitoa tu kama njugu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala pia la usimamizi, Mheshimiwa Rais aligawa pikipiki baada ya kufanya uzinduzi, baada ya kugawa zile pikipiki zimeenda site, pikipiki zile zinasimamiwa na watu wa TAMISEMI, hivi tunavyoongea haziendi site kwa sababu hawana mafuta, sijui kwako Spika Jimbo la Mbeya kama wanakwenda, tukija kwenye suala la bajeti tukisema jamani tunaomba hawa watu wasimamiwe na Wizara husika mnasema ooh! Sijui nini, sijui vitu gani! Mnatuvuruga na mnatuchanganya. Leo, sera ya kilimo inasimamiwa na Waziri wa Kilimo, tukienda kwenye utekelezaji anaekwenda kusimamia utekelezaji ni TAMISEMI! Huyu mtu ameharibu huku Waziri wa Kilimo hana uwezo wa kumwajibisha huyu Afisa anaesimamiwa na TAMISEMI huku chini, ni mpaka procedure tena Waziri wa TAMISEMI aingilie hapo ndiyo aende awajibike.

Mheshimiwa Spika, leo mafuta ya pikipiki, pikipiki zipo kule chini, Mkurugenzi anafanya shughuli zake kwa pikipiki zile zile ambazo zilitakiwa kwenda kufanyakazi ya kilimo, kwa hiyo kilimo kimebaki pale, Afisa Kilimo yupo pale, pikipiki haina mafuta, anatumwa na Mkurugenzi ambaye anapelekewa mafuta nenda kanifanyie kazi yangu fulani, tunaenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba Serikali ipitie upya mfumo wake wa kiutawala kuhusiana na suala zima kwenye Wizara hususani Wizara za kisekta za uzalishaji, kwamba wate hawa wa chini ni lazima watoke TAMISEMI nak ama hawatoki TAMISEMI basi tuone ni namna gani tuweke Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI atakaeshughulika na Wizara za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie pia suala la mifugo. Tumekuwa tukisafiri, tunatoka Mwanza mpaka Dar es salam, tumekuwa tukiona malori yameongozana yakiwa yamepakia ng’ombe hai anatolewa Mwanza ama Shinyanga anapelekwa Dar es salam kwenda kuchinjwa.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ajali nyingi zinazotokana na malori haya; madereva wamechoka ng’ombe wale wanapata ajali kule wanakufa na wengine wanakatika. Hatima yake hata hizo nyama tunazokula hazina afya kwa matumizi ya binadamu. Ng’ombe umemkeshesha siku tatu, wiki yuko barabarani, akifika apumzishwi anapitilizwa anaenda kuchinjwa; nyama ile inakuwa haina ubora kwa lishe ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, na umeeleza hapa kwamba Kamati ya Kilimo tumewaambia kwamba kuna udumavu wa samaki, je, sisi tunaokula inakuwaje? Je, tujiandae nasi kuwa wadumavu wa afya, kwasababu tunachokula tunajaza tumbo na hatuli chakula bora. Kwahiyo tuna lishe duni na naamini ndiyo maana hata tunaona hapa watu sijui ni kwasababu ya samaki wadumavu ndiyo maana tunaambiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipatia nami nafasi niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru hotuba ya Waziri Mkuu ukurasa wa 42 mpaka 43 umezungumzia suala la ardhi kama mtaji, pili kutokana na ardhi tuliyonayo kuwekuwa na migogoro mingi hali kadhalika nayo ameizungumzia kwamba sasa tunakwenda kwenye suala zima la utatuzi wa migogoro ili ardhi yetu iweze kutumika kama mtaji kwa maana kwenye sekta ya kilimo, sekta ya mifugo, sekta ya maliasili na sekta nyingine zote kwa sababu ardhi ndiyo kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya maneno mazuri yaliyoandikwa kwenye hotuba ya Waziri Mkuu, yamekuwa yakiandikwa kila hotuba ya kwake ya Waziri Mkuu lakini pia na ya kisekta kwenye Wizara zake husika. Tumekuwa tukizungumza suala zima la migogoro ya ardhi, Serikali imekuwa bado haituelewi, sijajua changamoto ni nini haswa, wanaona raha hiyo migogoro kuendelea kuwepo hapa nchini, ama kuna kitu wananufaika nacho kutokana na hii migogoro, sijaelewa! Wakija wataniambia kwa nini Serikali haitaki kutatua migogoro ya ardhi ya kiutawala lakini na migogoro ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji, migogoro ya ardhi baina ya maliasili pamoja na watumiaji wengine wa ardhi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chemba mgogoro baina ya maliasili pamoja na wananchi. Pori la Swagaswaga tumelizungumza, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili, Waziri wa TAMISEMI, Mifugo, Maji, kadhaa Mawaziri Nane walienda kwenye Pori la Swagaswaga, wakaenda wakazungumza na wananchi wakawaeleza hali halisi iliyoko pale. Wale wananchi wameanza kuishi pale kabla ya uhuru, wameishi pale kabla ya Serikali kwenda kuanzisha hifadhi, wameishi pale kabla hata ya uanzishwaji wa vijiji miaka ya 1970 huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali hiyo hiyo imejenga shule, imejenga zahanati, ni wapiga kura wanapiga kura pale, Serikali inawatambua, leo wakigeuka upande wa pili wa shilingi wanaambiwa ni wavamizi, mmevamia eneo la hifadhi, watu wanapigwa, watu wanauawa, watu wanafanyiwa manyanyaso ya kila aina, mpaka ubakaji unafanyika kwenye Hifadhi ya Swagaswaga. Hiki kitu siyo sawa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Mawaziri Nane imekwenda imepeleka wataalam, wamepeleka wataalam pale! Wataalam wameenda wamepima, kwa nini Serikali inakuwa na kigugumizi cha kutoa tamko la suala zima la wananchi wa Pori la Swagawaga kuendelea na maeneo yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu wamelima mmeenda kufyeka mahindi ya wananchi wangu, kwa sababu gani za msingi? yaani mtu mmemuacha anaenda analima, anapanda, mazao yanaota, yanakua, mnaenda mnafyeka siyo laana hiyo? Siyo laana hiyo?

MBUNGE FULANI: Ni laana!

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini mvua inyeshe? Kama Mwenyezi Mungu anatuletea mvua ya bure hatuilipii tunalima, tunapanda, mnaenda mnafyeka eti kisa hifadhi! Hivi tusipokuwepo leo hifadhi zitakuwa zina thamani gani? Tusipokuwepo binadamu hifadhi zitakuwa na thamani gani? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti kuna taarifa kutoka kwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wana muda wa kujibu wangetulia tu.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge anayeongea hivi sasa, kwamba sisi kama binadamu na hata viumbe waliopo hapa duniani tuna-balance kwa eco-system. Tusingeweza kuishi peke yetu bila kuwepo na wanyama, kuwepo na mimea, kuwepo na hifadhi, kuwepo na rasilimali zote zilizopo hapa nchini. Kwa hiyo, nataka kumpa taarifa kwamba hifadhi ni za muhimu asizione kama ni kitu ambacho hakihitajiki hapa duniani au hapa Tanzania.

Mhehsimiwa Mwenyekiti, pili nampa taarifa pia kwamba athibitishe kama kuna watu wameuawa, watu wamebaka, vinginevyo aondoe hii kauli.

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Kunti, taarifa hii unaipokea?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye ni Shahidi alikwenda Swagaswaga, mmefika pale mmeambiwa kwani mnachoficha ni nini? Hivi watu wale wananawake wanapoumia wewe unanufaika na nini? Lakini suala la kwamba eti tuna-balance tunahitaji, sawa tunaitaji tumepewa Mwenyezi Mungu ametupa hizi rasilimali ziweze kutusaidia na kutunufaisha watu wote sote, hawa wanyama wanufaike na sisi binadamu tuweze kunufaika. Leo kwa nini mnaona thamani ya mnyama kuliko binadamu? Kwa nini mnaweka thamani ya mnyama ni kubwa kuliko binadamu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Wizara wakija kuhitimisha waniambie mgogoro wa Swagaswaga unaisha lini Wilaya ya Chemba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la misafara ya Viongozi. Viongozi wetu tunawaheshimu na tunawapenda na tunajua changamoto kubwa wanazo kwa majukumu yao wanayoyafanya. Hivi kweli tunasema muda ni mali, wakati ni mali, kusimamisha wananchi zaidi ya masaa matatu barabarani, Kiongozi hajatoka atokako, tuna wagonjwa, tuna watu wanatakiwa kwenda kutekeleza wajibu na majukumu yao mbalimbali. Mimi ninaomba Viongozi wetu wanaosaidia hususan wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Polisi biashara ya kusimamisha wananchi mabasi sijui magari mengine na wananchi wengine watumiaji wa barabara kwa ajili ya viongozi wetu wanapopita waende kwa sababu wana mawasiliano. Wawe wanawasiliana kwa kadri muda unavyosogea wawe wanawaacha wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri Mkuu alikuwa natatoka nyumbani kwake kuanzia Saa Mbili na Dakika Kumi na Saba magari yamesimamishwa foleni imefika mpaka Nzuguni. Tunapandisha uchumi huo? Uchumi unapanda? Kusimamisha, sasa hiyo ni moja lakini je, fikiria hapa alikuwa anatoka hapo Mlimwa, kama Waziri Mkuu ameamua kutumia leo magari kutoka Dar es Salaam mpaka aje afike hapa Dodoma wananchi watasimama kwa muda gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana hivi vitu vingine hebu tuwe tunaenda na wakati na kwa safari ndefu niombe Viongozi wetu Wakuu watumie ndege waache kutumia magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye suala zima la maadili.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Taarifa.

MWENYEKITI: Kuna taarifa Mheshimiwa Kunti.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja.

MWENYEKITI: Kuna taarifa Mheshimiwa Kunti.

Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu.

T A A R I F A

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Wewe utakuja kujibu lakini. (Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Hapana Mheshimiwa Kunti si ungekaa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge, tunafahamu wote kwamba utaratibu wa utendaji kazi wa viongozi wetu umewekwa kwa mujibu wa taratibu mbalimbali ambazo zinasimamia pia heshima ya viongozi wetu hapa nchini.

Kwa hiyo, suala la namna ya ku–control hilo ni la watendaji ambao wako chini ya mamlaka zinazohusika. Kwa hiyo, nadhani ingekuwa ni bora tu kwa Mheshimiwa Mbunge kutoa ushauri kwa mamlaka zinazohusika badala ya kuhusianisha na utendaji kazi wa Viongozi wetu ambao umewekwa kwa utaratibu unaozingatia heshima ya Viongozi wetu pia hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tukiliweka hivyo litakuwa na logic nzuri zaidi kuliko kuendelea kusema Waziri Mkuu, kiongozi fulani. Tuende katika utaratibu ambao ni wa

usimamizi wa kiusalama na mambo mengine. Pia ni practice ambayo ipo katika ulimwengu mzima, practice ambayo imekuwa ikitumika katika kutoa heshima kwa Viongozi wetu na kuzingatia utaratibu ambao unatumika katika uendeshaji wa shughuli za viongozi na Serikali katika ulimwengu mzima. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti taarifa unaipokea.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mwongozo wa Spika.

MWONGOZO WA SPIKA

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mwongozo wako. Tunajua kwa mujibu wa Kanuni za Bunge, taarifa kuna muda maalum na imekuwa tabia ya Bunge hili Mawaziri kutumia muda wa Wabunge vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko kwenye kuchangia Bajeti kama wanataka kujibu, wasubiri kwa muda wao wa Kikanuni wa kujibu watapewa nafasi. Kama taarifa hatukatai lakini waende specific kwenye hoja na watumie muda wa Kiti vizuri.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti malizia mchango wako.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Bunge ni kuishauri Serikali, ndiyo tuko na wananchi kule chini, tunaona adha za wananchi, tunawashauri. Mkiona inafaa tekelezeni, mkiona haifai basi to hell haina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu maadili katika jamii yetu. Nilikuwa najiuliza kwa sauti nawaza, nikawa nasema hivi Serikali ina kila uongozi kule chini, kwenye Mtaa tuna Viongozi, kwenye Kata tuna Viongozi, kwenye Wilaya tuna Viongozi, kwenye Mkoa mpaka Taifa, hawa watu wanaosagana, hawa watu wanao sijui mwanaume anaenda anamngonokea mwanaume mwenzie, halafu ukiangalia hivi hii inaingiaje akilini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu wako kwenye mitandao tunawaona, wanajisifu, Serikali mpo. Wanadhalilisha Taifa letu, mmekaa kimya. Baraka, tukiona Wamachinga wako pale One Way, tunapeleka mgambo na polisi kwenda kuwachapa, wasagaji na wanaofanyana mambo ya ajabu ya kudhalilisha Taifa mmekaa kimya, hamsemi la heri wala la shari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Mama Massaburi anachangia, Mheshimiwa Mtemvu akasema na Wabunge tupo. Sasa nikawa nashindwa kushangaa, ndiyo maana hatuchukui hatua kwa sababu na sisi Wabunge tunafanyiwa haya maneno! Kama mimi Kunti nahusika, nafanywa na mwanamke mwenzangu; nafanywe na mwanamke mwenzangu? Inakuwaje? (Makofi/Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kunti, muda wako umeisha.

MHE. KUNTI Y. MAJALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ichukuliwe hatua. Biashara ya wanawake kufanyana na wanaume kufanyana wenyewe kwa wenyewe, ikome katika Taifa letu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu ambayo inatusababisha tuendelee kuishi.

Mheshimiwa Spika, Mkutano wa Pili wa Bunge hili, niliuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusiana na suala nzima la kilimo cha kutegemea mvua ya Mwenyezi Mungu. Waziri Mkuu majibu aliyoyatoa alisema kama Serikali inatoka sasa kwenye kilimo cha kutegemea mvua ya Mungu na kwenda kujikita kwenye kilimo cha tija, kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku za nyuma sekta ya umwagiliaji ilikuwa Wizara ya Maji lakini kwa kuona ufanisi wake ni mdogo tukashauri sekta ya umwagiliaji itoke kwenye Maji iende Kilimo ili watu wa Kilimo waweze kuisimamia sekta hii na iweze kuleta tija ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini cha kushangaza na cha kustaajabisha baada ya sekta hii kutoka Wizara ya Maji kuletwa Wizara ya Kilimo mwaka 2020/2021bajeti iliyoisha mwaka jana, Wizara ya Kilimo, Sekta ya Umwagiliaji Fungu Na.5 ilipitishiwa au iliidhinishiwa shilingi bilioni 17, fedha za maendeleo za ndani zilikuwa shilingi bilioni 3 na fedha za nje zilikuwa ni shilingi bilioni 9. Sasa katika hizi fedha za ndani shilingi bilioni 3 Serikali haijatoa fedha hata shilingi moja kwa ajili ya kwenda kwenye umwagiliaji na badala yake fedha za nje wenzetu wakatoa shilingi bilioni 5. Tunasema Serikali tunakwenda kujikita kwenye kilimo chenye tija cha umwagiliaji mnatenga wenyewe bila ya kulazimishwa mnasema hii ndiyo tutakayoiweza hata kuitoa nako ni shughuli, imeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najiuliza kama Bunge tuna sababu gani ya kukaa humu ndani na jadili na kupitisha fedha halafu haziendi kwenye kazi ambayo tumekwenda kuipitisha? Leo Fungu Na.5 linaomba fedha za maendeleo shilingi bilioni 5, shilingi bilioni 3 haikupewa shilingi bilioni 5 itapewa? Hivi vitu vinakwaza, vinakatisha tamaa, vinaturudisha nyuma na wakati mwingine tunaona hatuna sababu ya kuendelea kuchangia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inakiri kwamba sekta hii ndiyo ambayo imeajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania. Hivi inasema imeajiri kwa wakulima mmoja mmoja kuhangaika huko kwa majembe ya mikono, kwa mikopo ya gharama kubwa, ilhali tuna Benki yetu ya Kilimo ambapo lengo na madhumuni ilikuwa ni kwenda kuwasaidia wakulima wetu kuweza kupata fedha na mitaji kwa ajili ya kuhakikisha wanakwenda kulima kilimo chenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe kwa Serikali kwa kuwa Benki ya Kilimo iko chini ya Benki Kuu ambayo masharti yake yanakwenda kubaki vilevile kama benki nyingine, tuone namna gani tunakwenda kuitoa Benki hii ya Kilimo ili tuweze kuipunguzia masharti wananchi wetu waweze kupata mikopo ya yenye tija na hatimaye waweze kilimo chenye tija.

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa naipokea.

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba Wizara ya Kilimo wana Mfuko unaitwa Agriculture Trust Input Fund ambapo ni mfuko huu, pamoja kwamba ni mfuko chini ya Wizara uko one hundred percent commercial. Wanamkopesha mkulima anayetegemea mvua, wanamkopesha mkulima ambaye hapati masoko lakini katika kipindi cha miaka minne ambayo wamempangia kurejesha akisharejesha anakuta kuna interest ambayo inazidi asilimia 50 ya hela halizokopa. Kwa hiyo, matokeo yake watu wengi wanaona hakuna tofauti ya hela inayosimamiwa na Wizara ambayo ilipangwa kwa ajili ya kuwasadia wakulima na ile inayotoka kwenye benki za biashara.

Mheshimiwa Spika, nakushuru sana.

SPIKA: Mheshimiwa Kunti unapokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nimshukuru kaka yangu Mheshimiwa Kanyasu, haya yote ndio tunayazungumza suala zima la kumsaidia mkulima, Serikali dhamira na nia yenu ni kuwasaidia wakulima kuweza kuhakikisha wanakwenda kupata fedha ama mikopo yenye riba nafuu na itakayokwenda kutolewa kwa muda mrefu hili waweze kuhakikisha kwamba wanalima mazao yao na wanapata fursa ya kuweza kuyauza kwa tija na hatimaye waweze kurejesha hiyo mikopo.

Mheshimiwa Spika, lakini stakabadhi ghalani Waheshimiwa Wabunge wenzangu hapa wamesema suala zima la stakabadhi ghalani na Mkoa wangu wa Dodoma tuliathirika sana na wakati wizara inatulekea stakabadhi ghalani Mkoa wa Dodoma, Mheshimiwa Bashe alituita pale ukumbi wa Msekwa tulimkatalia tukamwambia stakabadhi ghalani kwa kuwa Serikali hamjajipanga kuleta stakabadhi ghalani kwa kuwa wananchi wetu hawana taarifa hawaelewe ni chochote. Lakini pili hamjaweza kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Dodoma na mpaka mfikie hatua ya kwenda kutuletea stakabadhi ghalani.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wao wana mabavu, wana vyombo vya dola wana kila kitu wakaamua kutuletea stakabadhi ghalani watu wetu walipigwa walinyanganywa mazao yao lakini pili mbaya zaidi Wilaya ya Chemba, Kata ya Mpendo tunapakana na Bahi shughuli zote na kata ile ndiyo inayolima ufuta kwa wingi Kata ya Mpendo wanapata huduma Wilaya ya Bahi, wakulima wa Mpendo walikuwa mazao yao wakivuna wanapeleka Bahi wanauza.

Mheshimiwa Spika, baada ya stakabadhi ghalani kwa kuwa zoezi hili lilikabidhiwa kwa Wakuu wa Wilaya wananchi na wakulima wa Kata ya Mpendo walikuwa wanalazimishwa awe ana kilo mbili awe ana debe moja awe na gunia atoke Mpendo kilometa 97 mpaka Makao Makuu ya Wilaya ya Chemba pale kwenye ghala aende akaweke bodaboda ukikodi ni shilingi 35,000, kilo ya ufuta ni shilingi 2,000 ana debe moja ni Shilingi 40,000huyu mkulima mnamuinua kwa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana stakabadhi ghalani wabaki nayo wao Bashe aipeleke kule pamoja na Mheshimiwa Mkenda pelekeni kwenye majimbo lakini kwetu kwenye Mkoa wa Dodoma tunawashukuru kwa huduma hiyo lakini hatuhitaji hata kuisikia na nitakuwa wa kwanza kwa ajili ya stakabadhi ghalani sitaki kusikia stakabadhi ghalani sitaki kusikia stakabadhi ghalani ndani ya Mkoa wangu wa Dodoma. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru nami kwa kunipatia nafasi niweze kusema yale yanayojiri kwenye Wizara hii. Kati ya Wizara ambayo tuliitegemea na Watanzania wameendelea kuitegemea kwa ajili ya kuongeza ajira; na pili, kwa ajili ya kuongeza uchumi wa Watanzania na uchumi wa Taifa letu ni Wizara hii ya Uwekezaji, Viwanda pamoja na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala zima la viwanda na ambalo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema. Mwaka 2022 Serikali ilihamasisha Watanzania wa Mikoa mitatu; Dodoma, Singida na Simiyu, kwenda kuwa Mikoa ya Kimkakati ya kulima zao la alizeti ili tuweze kuondokana na wimbi kubwa la uingizaji wa mafuta kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walihamasika na wakaomba ili waweze kutekeleza mkakati huo wapatiwe mbegu na vitu vingine. Pamoja na changamoto zote zilizokuwepo kwenye upatikanaji wa mbegu na pembejeo, wananchi hawa walifanya. Vile vile wakati tunapitisha bajeti, tuliondoa kodi kwenye mafuta kutoka nje ya nchi. Wananchi wetu wakalima alizeti, watu wa viwanda vya kuchakata mafuta, wameamua kupunguza bei ya mazao ya kuchakata mafuta hususan zao la alizeti. Baada ya kupunguza bei, wananchi wanaona hakuna sababu yoyote ya kuendela kulima zao la alizeti ambapo wanatumia gharama kubwa kwenye uzalishaji, likija suala zima la mapato, hawapati kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kisingizio wanachokileta leo na Mheshimiwa Waziri amekisema eti kwamba watu hawa wamefunga viwanda kwa sababu ya ukosefu wa malighafi za viwanda vyao. Hivi leo nani anaeweza kwenda kulima atumie laki tano kwenye heka moja aje avune magunia 20 aende akauze kwa elfu Sitini? Ni nani huyo anaeweza kufanya kitu cha namna hii? Kwa hiyo, kosa ni la Serikali ambao ninyi wenyewe mnaleta hapa mnatushawishi Wabunge tupunguze kodi kwenye mafuta halafu mnaendelea kutoa vibali vya mafuta.

Mheshimiwa Spika, leo wafanyabiashara wote wa Sekta ya mafuta ya kula wameamua kuagiza mafuta nje kwa sababu kodi yake ni ndogo na faida yao ni kubwa, mazao ya alizeti yanateseka mtaani yako kule wananchi hawana mahali pa kupeleka. Sasa, kwa nini tunafikia kwenye hatua hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuanagalia kwenye viwanda vyenyewe bado hatuna viwanda vya kutosha ndani ya taifa letu. Leo ninapozungumza hapa Serikali yetu ama nchi hii hatuna viwanda vya kutengenezea hata vifungashio. Leo vifungashio vya kila zao tunatoa Kenya, vifungashio hivyo zao la Parachichi leo box tunachukua Kenya na wananadika Product from Kenya wakati parachichi inatoka Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mchele leo wa Kyela Kifungashio kinatoka Kenya unaandikwa ni mchele wa Kutoka Kenya wakati ni mchele wa kutoka Tanzania Kyela. Hivi hata vifungashio? Viwanda leo tuna mashamba ya miti yako pale Iringa ya kutengeneza makaratasi ndio tunaagiza vifungashio kutoka Kenya? Waziri, tunakuomba tafadhari kama kuna sehemu ambayo unatakiwa uwekee mkazo ni kukuza na kutangaza bidhaa zetu. Anza na viwanda vya vifungashio, tangaza nchi yako, tangaza bidhaa yetu ili tuweze kuondokana na huu urasimu ambao tunafanyiwa na nchi za wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la leseni. Imekuwa ni muda sasa na ni changamoto kubwa kwa wananchi na wafanyabiashara wetu wadogo wadogo kule chini. Leseni unakata lakini unatakiwa kuihuisha kila mwaka kitu ambacho kinakuwa ni kero kwa wafanyabiashara wetu. Hata hivyo, kila ninapouliza naambiwa suala la kuhuisha leseni ili kuwatambua wafanyabiashara waliopo kwenye eneo husika ama tulionao nchini. Nikawa najiuliza hivi ni kwa nini Vitambulisho vya Taifa hatuhuishi kila mwaka ili tujue nani kafa, nani yupo, nani kahama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama suala ni kutambua na kujua kwa nini vya taifa hatuhuishi kila mwaka? Leseni ambayo watu hawa wanajenga uchumi wa Taifa lao, wanalipa kodi kwa Taifa lao, leseni wanalipia lakini leseni hiyo kila mwaka umsumbue mwananchi huyu Kwenda kupanga foleni Manispaa kutafuta leseni. Hata hivyo, kwenye suala la leseni hilo hilo, tulisema hapa mfanyabiashara anaeanza biashara asikadiliwe kodi mpaka kipindi cha miezi sita afanye kwanza biashara. Kinachofanyika kwa uhalisia ulioko huko chini sio kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili upate TIN ni lazima uwe na leseni ambayo umetoka nayo Manispaa. Ukiwa na leseni ukienda kupata TIN ni lazima ukadiliwe. Vilevile, wanakukadilia kwa miezi hiyo ya huko nyuma. Kwa hiyo, ukishakadiliwa ni lazima ulipe hakuna namna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu mfanyabiashara akishindwa kulipa anaandikiwa deni. Hilo deni linakwenda mwisho wa siku mnakwenda kufunga biashara za wafanyabiashara na mara mnapeleka kesi Mahakamani, kuzimaliza hamzimalizi, watu wanaendelea kufirisika ndani ya Taifa hili, halafu tunasema tunataka kutengeneza mabilionea wa Tanzania. kwa mfumo tulio nao hakuna mabilionea ni masikini wa Tanzania watanendelea kutngenezwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe kwenye suala la Leseni Mheshimiwa Waziri, wasaidieni watanzania kupata leseni iwe ni mara moja. Kama kuna michnago, kwanza michango kwenye biashara ziko lukuki, msimsumbue tena kaleseni kila mwezi, kila mwaka anaenda kuhangaika nako. Wekeni mfumo ambao utamsababisha huyu mwananchi akate leseni hata ndani ya miaka mitano afanye biashara akiwa na uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukadiliaji wa mapato TRA. Suala la ukadiliaji wa mapato pia nalo ni changamoto. Mtaji wangu ni kidogo, ukifika TRA kwanza unaulizwa eneo lako la biashara ni la kwako binafsi ama umekodi? Kama umekodi unaulizwa kiasi gani? Mtaji wako unaoanza nao biashara ni kiasi fulani. Nimefanya biashara nikifika wakati wa makadilio ya biashara ninakadiliwa kuanzia mtaji wangu mpaka na faida. Hii sio haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unachukuaje? Mitaji yenyewe tumekopa benki. Wajasariamali wetu hawa, wafanyabiashara wetu wanaenda kukopa benki. Kwa hiyo, unapomkadilia mpaka mtaji wake humtendei haki. Tumekuwa tukisema hapa biashara siku zote ili niweze hata kulipa mkopo wangu benki na kufanya mambo mengine tunatumia faida sio mtaji. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, pamoja na Wizara ya Fedha suala la kulipa kodi kwa wafanyabiashara tu-charge kutokana na faida sio kujumlisha na mtaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa Kituo Jumuishi (One stop Center). Tumekuwa tukisema pia hili jambo kila wakati, iwe ni wawekezaji wetu lakini hata wafanyabiashara wetu wadogo wadogo. kumekuwa na changamoto sana. Wizara ya Madini wameweza, Mheshimiwa Dada yangu Ashatu, wewe unashindwa nini mama? Tusaidieni, wasaidieni wafanyabiashara wekeni kuwe na eneo moja dirisha moja. Watu hawa wakifika lile eneo aingie dirisha la kwanza atoke, aingie la pili atoke, aingie la tatu atoke badala ya changamoto leo anazozitumia mfanyabiashara. Anatakiwa kwenda TRA, manispaa, benki, OSHA, aende sijui nani… vurugu anatumia siku tatu, wiki, miezi hajakamilisha hiyo michakato. Kwa hiyo, tunaomba pia wewe kama walivyofanya Wizara ya Madini, halikadhalika Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara tusaidieni hilo jambo ili tuweze kuwasaidia hawa wafanyabiashara wa kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ucheleweshaji wa Vibali vya wawekezaji. Wawekezaji wetu wengi wamekuwa wakija nchini lakini kumekuwa na urasimu sana. Tuombe angalieni Kanuni zetu, Sheria zenu. Tunatambua mnataka kupata wawekezaji wenye uhakika ndani ya Taifa letu. Punguzeni huo mlolongo, punguzeni kuvuta vuta miguu. Twendeni tufanye kazi tukimbizane na speed ya Mheshimiwa Rais, anayoifanya ili tuweze kupata wawekezaji wa kutosha watakaoleta tija ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba nizungumzie na mimi suala la Sakata la Twiga pamoja na Tanga. Mheshimiwa Waziri, utanisaidia tu, nilikuwa najiuliza hivi kama Tanga amefirisika na anaona hawezi tena kuendelea na hii biashara, kwa nini achague mtu wa kumuuzia hiyo biashara yake? Kwa nini? Pia ninataka nijue hivi anachagua yeye ama Serikali ninyi ndio mnamchagulia mtu wa kununua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Kunti nimefirisika kwenye biashara yangu sioni dalili huko mbele za kuendelea na hii biashara si natangaza? Kwamba biahara hii siwezi kuendela nayo natangaza nauza hii biashara ili nipate watu wengine mbadala tofauti, waje hapa kama ni mnada nipige mnada nipate kile ambacho ninakihitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini leo tunasimama na msimamo wa kwamba Twiga ndio aende akanunue Tanga? Ninapata shida ukija hapa uniambie. Kwa nini mnalazimisha Twiga amnunue Tanga Cement? Nataka hayo majibu yenye kina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa wakati wako. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii nyeti. Nawapongeza watani zetu Yanga, kwa jitihada kubwa walizozionesha kwa kuliwakilisha Taifa vizuri. Hongereni sana. Hicho wana Simba ndicho tulichokuwa tunakitaka, msiwe mnadandala dandala tu, pigeni mzigo, boli litembee, mlete ushindi na heshima ya Taifa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo. Maji ni afya, maji ni biashara, maji ni chakula, maji ni dawa, maji ni kila kitu. Nianze na Jiji la Dodoma. Nitambue jitihada zinazoendelea za kwenda kupata maji safi na salama yenye uhakika kwa jiji la Dodoma. Jitihada hizi bado hazileti matumaini kwa wanajiji wa Dodoma kulingana na miradi iliyowekwa ambapo miradi hiyo ni mikubwa na itatekelezwa kwa muda mrefu. Kwa hiyo, maana yake nini? Wanajiji la Dodoma bado tutaendelea kuteseka na ukosefu wa maji ya uhakika ndani ya jiji hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiji la Dodoma lina mradi unaotarajiwa kuja kumaliza changamoto ya maji Dodoma ni Farkwa. Pia tuna mradi wa Ziwa Victoria. Miradi hii yote haiishi leo wala kesho, ni zaidi ya miaka sita. Nikawa najaribu kufikiria, kama miradi hii inatupeleka miaka sita, hiyo ni michache, labda mpaka nane, kumi, jitihada gani za Serikali kwa Wizara yako inayokwenda kuzifanya kwa ajili ya kuhakikisha tunapata maji safi na salama na yenye uhakika kwa kipindi hiki ambacho ninyi mnaendelea na michakato hiyo kwa ajili ya Ziwa Victoria pamoja na Farkwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba kuna visima Nzuguni mmechimba. Vile visima mbona navyo vinachukua mchakato wa muda mrefu? Tangu tumekwenda kutembelea mwaka 2022 mpaka leo kuko kimya. Tunaomba hiyo miradi ikamilike mpunguze hiyo jam kwenye Kata ya Nzuguni, Kata ya Ipagala na Kata ya Kisasa ili yale maji yaliyokuwa yanatoka Mzakwe kuja kwenye hizi kata yaweze kugawanyika yaende kwenye maeneo mengine. Wizara toeni fedha, mpeni Mkandarasi asambaze maji kwenye vile visima ili tupunguze hiyo adha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, mchakato wa Ziwa Victoria, upembuzi wa awali umekamilka, Farkwa, halikadharika, hivi ni nini kinachosuasua mpaka leo? Naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja utawaambia wana Dodoma changamoto ambayo bado ipo inayosababisha kutokuendelea na miradi hii miwili ni nini? Nitaomba uje uwaambie wanajiji la Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri, miji 28, Waheshimiwa Wabunge wamesema; Chemba Mkandarasi ameripoti, amefika, lakini Mheshimiwa Waziri Mkandarasi huyu karipoti. Jimbo la Chemba lina vijiji 114, kata 26, na vitongoji 436. Jimbo hili kati ya vijiji 114 lina vijiji 47 tu vyenye maji. Vingine vilivyobaki havina maji. Tunatarajia na tunaendelea kutarajia na kuiomba Serikali kubadilisha mtazamo wa maji ya Farkwa kutokuja Chemba, kwa sababu mtakuwa hamtutendei haki. Mradi huu wa miji 28 unakwenda kutekelezwa Chemba na viunga vyake. Ina maana tutatekeleza kwenye vijiji visivyozidi vitano. Kwa hiyo, jumlisha 47, tutakuwa na vijiji 52. Angalia huo upungufu wa maji kwa Wilaya ya Chemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunatamani na tunawaomba sana, mradi wa Farkwa, maji tupate na sisi wana Chemba, ndiyo suluhisho letu, badala ya kutuambia, mnatoa maji Farkwa, Wilaya ya Chemba ambako ndiko maji yanakozalishwa, mje myapitishe yaende Bahi, yaje Chamwino, yaje Dodoma Mjini, Chemba tubaki tunatazama tunapiga picha. Hatutakubali hicho kitu mkifanya kwa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hali ya kuondokana na changamoto ya maji kwenye Wilaya ya Chemba, ulitupatia mabwawa matatu; mabwawa mawili yamekamilika. Tuna suala la bwawa la Kiboka, Mkandarasi alileta certificate tangu mwaka 2022 mwezi wa Kumi na Moja, hamjampa advance payment. Tunaomba huyu Mkandarasi apewe advance payment aweze kwenda site aanze mradi ule ili nasi tuondokane na hiyo adha ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitambue jitihada kubwa za mamlaka zetu za maji zinazofanya huko kwenye Mikoa yetu na kwenye Wilaya zetu. Katika jitihada hizo zote mamlaka za maji wanazozifanya, bado wana changamoto kubwa ya ukusanyaji wa madeni kwa watumiaji wa maji. Kwenye hili Waziri nitakuomba, Mamlaka zako naomba uzisimamie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi sana naomba nizitaje chache kuhusiana na madeni haya. Naomba nianze na mamlaka RUWASA, imeshindwa kukusanya Shilingi milioni 119, ziko huko, hawajakusanya wao; DUWASA Shilingi bilioni 207; SUWASA Shilingi milioni 532; KUWASA, Shilingi bilioni 1.7; MUWASA Shilingi bilioni nne; DUWASA Shilingi bilioni 6.7; MWAUWASA Shilingi bilioni 6.9 na DAWASA Shilingi bilioni 11. Hizo chache! Jumla kwa haya madeni yote ukijumlisha ni Shilingi bilioni 31.6. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hii laiti ingekusanywa vizuri, ingetusaidia kuwasaidia na wenzetu wengine wa vijijini kuhakikisha nao tunawaboreshea mazingira bora ya upatikanaji wa maji safi na salama ya kunywa. Wanafanya kazi kubwa, tunaitambua, lakini tunaomba uwasimamie waongeze jitihada ya ukusanyaji wa madeni kwa watumiaji maji kwenye maeneo yao waliyosambaza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, tasisi za Serikali zinazodaiwa na mamlaka ya maji pia tuziombe zilipe madeni yao zimalize ili taasisi hizi ama mamlaka zetu hizi, ziweze kujiendesha na ziendelee kutoa huduma za maji kwa watumiaji wengine wa maji ambao mpaka sasa bado hawajapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la majitaka kwa Jiji la Dodoma na majiji mengine. Bado tuna changamoto ya majitaka katika nchi yetu na hususan Jiji la Dodoma. Niliona jana Mheshimiwa Waziri ukisaini mikataba kwa ajili ya mchakato sasa wa kwenda kuhakikisha tunaanza miundombinu ya uondoaji wa majitaka ndani ya Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, speed ni ndogo, kutoka asilimia 20 mpaka kufikia asilimia 40, Mheshimiwa Waziri tunaomba mpambane. Hizi fedha ambazo leo DUWASA wameshindwa kukusanya Shilingi bilioni sita, na pia kuna upotevu wa maji yanapotea huko barabarani kutokana na miundombinu mibovu; hizi fedha wangekusanya wangeweza kusaidia pia kwenye suala la uwekezaji kwenye miundombinu ya majitaka na hatimaye Jiji hili likaendelea kuwa safi na watu tukaepukana na maradhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, speed wanayokwenda nayo ya kwenye suala zima la majitaka tunaomba waiongeze, ni eneo ambalo wamelisahau sana. Kwa hiyo, tunawaomba sasa twendeni kwenye suala zima la uwekezaji wa majitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine ambalo nilitamani kulisemea ni suala zima la upandishaji wa bill za maji. Kumekuwa na utaratibu wa mamlaka zetu kwamba wanakwenda, wanaona gharama za uendeshaji zimekuwa kubwa na kuamua kupandisha bili za maji. Wamekuwa wakitumia mfumo wa kutuma ujumbe kwenye simu za wateja ili kwenda kushiriki kwenye vikao vya kupandisha maji, lakini taarifa zile, na huu ni mkanganyiko wa hizi taasisi; anayetaka kupandisha bili ya maji, tuseme ni DUWASA, lakini kibali anatakiwa apewe na EWURA, Wizara ya Nishati. Sasa huyu anayetakiwa kupewa kibali ili aweze kupandisha gharama ya bili za maji, yeye ndiye anayealika wajumbe ama wadau wa watumiaji maji kwenye huo mkutano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano mmoja. Mwezi uliopita, mimi binafsi na baadhi ya Wabunge tulipata message.

MBUNGE FULANI: Mmh!

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Saa 7.00 mchana ndiyo tunatumiwa message za kwenda kwenye kikao kesho, lakini ukiangalia hata hizo jumbe zenyewe namna zilivyotumwa, siyo rafiki sana. Nikawaza kwamba aidha, kuna mbinu inayochezwa baina ya EWURA pamoja na DUWASA ili watumiaji wa maji wasiende wengi ili wao wapitishe kile wanachokihitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Wizara ya Nishati na Wizara ya Maji, suala la kupata maoni kwa ajili ya kupandishwa bili za maji, wasiwe wanaalika mkutano wa hadhara wa kuja kukaa JK pale, waende chini kwa watumiaji wetu wa maji kule walikopeleka mita. Tuwaitishe mikutano; tuna taasisi zetu, tuna mifumo ya kitawala. Tuna Mwenyekiti wa Mtaa, Mwenyekiti wa Kijiji, tuna watendaji wako kule, wawape taarifa, waweke kipaza sauti, wawatangazie wadau wa maji, ili waende wakatoe maoni yao kuhusiana na sula zima la kupandisha bili za maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naitolea mfano Dodoma kwa sababu ndilo eneo ambalo nina uzoefu nalo. Dodoma leo tunapandishiwa maji, lakini kutokana na hali halisi tuliyonayo ya mgao wa maji, kwa mwezi tunapata maji siku nane. Siku nane ndizo tunazopata maji, sasa unataka unipandishie bili tena, kwa hiyo, unajikuta unaanza kuwaza, kama maji siyapati, kwa nini unataka kupandisha bili? Kwa hiyo, kwenye hili, nawaomba sana Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Nishati, angalieni namna bora na msiwe mnaona tu, wakati mwingine Mheshimiwa Aweso, haya madeni mamlaka zikusanye, ziache kukimbilia tu kwenda kupandisha bili, kuwaongezea wananchi mzigo. Wakusanye madeni yao, waboreshe mabomba yao ili upotevu wa maji usiwepo, maji yapatikane vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwa Mheshimiwa Waziri, ili kuondokana na hizo gharama za madeni, tulikuomba hapa pre-paid meter. Lete pre-paid meter. Mmefunga kwenye baadhi ya taasisi, tunaomba na Watanzania wengine tupeni. Zipe mamlaka ziagize pre-paid meter wafungiwe watu. Moja utapunguza hata watumishi ndani ya Wizara, kwa sababu umeme leo tunalipa ndiyo tunatumia, kwa nini maji tusilipe ndiyo tutumie? Tutaondokana na migogoro, na kusuguana na kunyoosheana vidole kusikokuwa na tija. Utaondokana na malalamiko ya ubambikizaji wa bili, utaondokana na malalamiko ya kila aina. Tutafutie pre-paid meter zitazoenda kutuletea ukombozi katika suala zima la ukusanyaji wa mapato ndani ya Wizara yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. Nakutakila kila la heri Mheshimiwa Aweso katika utekelezaji wa majukumu yake pamoja na watendaji wake wote, Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru nami kwa kunipatia wasaa ili niweze kutoa mchango wangu kwa Azimio hili. Nitambue pongezi zilizotolewa na Wabunge wenzangu pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Kamati yetu. Kwa hiyo, nami niunge mkono tu pongezi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Azimio hili lina mawanda mapana na linatuonesha dira kama Taifa na manufaa mapana na makubwa ndani ya Taifa letu. Pamoja na hayo manufaa makubwa yanayoonekana kwenye hili Azimio, kuna mambo kadhaa ambayo kama nchi, kama Serikali lazima wayaangalie kwa jicho la kipekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaomba kuyasema machache. La kwanza ni suala zima la biashara zetu za ndani kwanza. Leo biashara ndani ya nchi, bado kuna purukushani nyingi sana kuhusiana na suala zima la sheria, kodi na mambo kadha wa kadha. Sasa tunapokwenda kujiunga kwenye jumuiya hii ni lazima tuone: Je, hivi sisi kama nchi, changamoto zetu ndani ya nchi kwa wafanyabiashara wetu tumezitatua kwa namna gani? ili tunapotoka huko kwenda kushindana na wenzetu ili tuweze kuona sasa huku ndani tumemaliza, sasa tunakwenda nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema suala la leseni. Leo ndani ya Taifa letu tuna leseni; nikiwa nauza mandazi, natakiwa niwe na leseni, nina guest house, niwe na leseni, nina magari kama Waheshimiwa Wabunge walivyosema, lazima niwe na leseni ya magari, sijui nauza duka, lazima niwe na leseni ya duka. Hivi vitu wakati mwingine hebu kama Taifa tujitathmini. Kuna faida gani ya mfanyabiashara mmoja kuwa na leseni saba? Kuna faida gani ya mfanyabiashara Kunti kuwa na leseni saba za biashara? Hivi ni kwa nini kama nchi tusione kuna sababu sasa ya kutoka huko? Kama ni issue ya mapato ya Halmashauri, Serikali itengeneze mfumo kwamba mfanyabiashara awe na leseni moja, na Halmashauri itapata mapato yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Serikali, tutakapoingia kwenye hili Azimio, tunapojiunga ni lazima tutoke sasa kwenye ule mfumo wa kuwa na leseni saba, tutengeneze mfumo wa kuwa na leseni moja ili pia hata hao wenzetu wanaokuja wakute tumeshajipanga kama nchi, tuko serious na tunajua nini tunachokifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Azimio watakaokwenda kuwajibika ni wafanyabiashara ama ni sekta binafsi na siyo Serikali. Kwa hiyo, ni lazima tutengeneze mazingira rafiki ya kuwa karibu na sekta binafsi na kuwatengenezea mazingira rafiki yatakayoweza kufanya kazi ama kufanya biashara zao bila usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu hapa kuna Wizara mbalimbali ambazo kila Waziri anasimamia sera yake kwenye Wizara yake. Nafahamu Mheshimiwa Waziri ni mratibu kwenye suala la biashara. Sasa kama nchi, ni lazima Serikali muanze iwe na lugha moja. Bila ya kuwa na lugha moja, leo Waziri wa Nishati anasimama na ya kwake, Waziri wa Kilimo anasimama na ya kwake, Waziri wa Fedha akija hapa ana ya kwake, Waziri wa Habari ana ya kwake, Waziri wa Biashara nawe unakuja na story zako, hatutaeleweka kama Taifa na itifaki hii haitaleta tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ifike wakati pia kama Serikali, kama nchi, ni lazima muanze kuongea lugha moja. Atakachokisema Waziri wa Viwanda akiseme Waziri wa Fedha; atakachokisema Waziri wa Fedha vivyo hivyo Waziri wa Nishati, Serikali tuweze kuwa na lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye itifaki hii pia ni lazima tuandae rasilimali watu wenye ujuzi kwenda kushindana na hawa wenzetu. Tusipoandaa rasilimali watu yenye ujuzi, suala la uwepo wa ongezeko la ajira kwenye nchi yetu itakuwa ni ndoto za Abunuasi. Ajira zitachukuliwa na mataifa ya wenzetu na sisi tutabaki kuendelea kulalamika. Kwa nini? Ni kwa sababu kama Taifa hatukuchukua hatua kuwaandaa watu wetu. Kwa hiyo, ni lazima tuandae rasilimali watu ambao wana ujuzi ili tuende tukashindane na hizo fursa za ajira ikiwezekana tuzibebe nyingi zaidi kwenye Taifa letu tuweze kupunguza hilo wimbi la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni ubora wa huduma. Lazima huduma zetu ziwe na ubora, zikidhi viwango vya mataifa hayo mengine. Tusipokidhi ubora wa huduma zetu pia itakuwa ni changamoto, tutabakia kupokea huduma za watu kutoka kwenye hayo mataifa na sisi tutakuwa na shimo la taka la kujaza matakataka humu ndani ya nchi. Kwa hiyo, lazima tujipange kuwa na huduma ya ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tu mfano mdogo sana ambao ulinipata jana. Jana kulikuwa na shida ya umeme, ulikatika na baadaye umeme uliporudi, kukawa na maeneo umeme upo na maeneo mengine umeme haupo. Mimi nina namba mbili za emergency za TANESCO, nikapiga namba ya kwanza; cha kwanza cha kusikitisha, yaani ile namba ya simu ukipiga, kabla hujahudumiwa, tayari hela imeshaanza kutumika. Kabla hujahudumiwa, wameshachukua hela, halafu hiyo ni namba ya huduma ya mteja anayetakiwa kupewa huduma, unamkata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimepiga namba ya kwanza haikupokelewa, namba ya pili haikupokelewa, nikarudia. Namba ya kwanza ikapokelewa. Ilivyopokelewa nikapewa namba ya usajili wa tatizo nililoripoti, nikaambiwa baada ya nusu saa nitapata huduma. Sikupata hiyo huduma. Nikapiga ile namba ya pili, ikapokelewa, nikapewa namba nyingine tena ya huduma. Yaani taasisi hiyo hiyo moja, kwenye mfumo pale hawezi hata kuona kwamba mita namba hii imeshapewa namba ya huduma hii, tatizo lake linashughulikiwa. Nikapewa tena namba nyingine ya huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaona ni namna gani ambavyo kama nchi, hata mifumo yake tu yenyewe bado haijawa bora. Haiwezekani kitengo cha huduma kwa wateja, emergency call unapiga namba mbili unapewa majibu tofauti na watu tofauti na wako kwenye system. Nilifanya makusudi tu kupiga, niliamini angenijibu akaniambia tatizo lako limeshapokelewa, linafanyiwa kazi, lakini cha ajabu nikapewa namba nyingine tena nikaambiwa subiri nusu saa. Kwa hiyo, tuone changamoto zilizopo kwenye huduma zetu tunazozitoa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna Bwawa la Mwalimu Nyerere lile pale ambapo tutakwenda kuzalisha umeme ambao utahudumia Watanzania, tunatarajia tuwauzie na wengine. Kama changamoto hata za kwenye mfumo ziko hivi, nani atachukua huo umeme wetu? Hayupo. Kwa sababu watachoka, mtakuwa hamwasikilizi, mnawapa maneno, badala ya kuwapa huduma inayostahili. Kwa hiyo, lizingatiwe pia suala zima la ubora wa huduma zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni matangazo. Tunaweza tukawa na hizo fursa nyingi lakini tusipozifanyia matangazo ya uhakika, yenye tija, pia hali kadhalika hakuna atakayeweza kujua sisi kama Taifa la Tanzania tuna vitu gani ambavyo vinaweza vikaingia kwenye soko hilo la ushindani huko kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala zima la amani ndani ya nchi yetu. Yote haya tunayoyafanya ni lazima kama Taifa tuwe na amani ambayo itaweza kutusaidia…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Jenista.

TAARIFA

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa mchango wake na amezungumza hapa jambo la msingi sana. Changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza kwenye sekta mbalimbali katika kutoa kuhuduma, biashara hizi za huduma na ametoa mifano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimpe taarifa kwamba kwa kuzingatia maelekezo ya Bunge hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Serikali yetu kwa kuzingatia usikivu wa Serikali yetu. Bunge lilitushauri kuanzisha sasa kitengo ama idara maalum ya monitoring and evaluation ili kadhia zote zinazojitokeza, ikiwemo kama hii, changamoto za kimfumo katika utoaji wa huduma fungamanishi Serikali iwe na majibu ya jumla na hasa kupitia kwenye mamlaka zetu na hasa mamlaka ya Serikali mtandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakubaliana naye na naomba tu nimpe taarifa kwamba jambo hili tumeshaanza kulifanyia kazi, idara imeshaanzishwa, uratibu unafanyika na huko tunakoingia kwenye protocol ya SADC haya ni mambo ambayo tulishayaona na tumeshajipanga ili iwe ni sehemu ya utatuzi wa changamoto tunazozipata. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Kunti unaipokea taarifa hiyo, uendelee na mchango wako?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nahisi Mheshimiwa Waziri hajanielewa.

Pili, kazi yangu mimi Mbunge na wajibu wangu ni kusema yale tunayoyaona na tunayokutana nayo na tunayoambiwa na wananchi, na kazi yao kama Serikali ni kusikiliza yale tunayoyasema yanayotoka kwa wananchi. Sasa suala la tatu, mkiamua kuyafanyia kazi ni juu yenu, mkiamua kuyapuuza ni hiari yenu. Kwa hiyo, mimi kama Kunti, Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimetimiza wajibu na jukumu langu ndani ya Taifa langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee. Amani ndani ya Taifa letu. Hii amani tuliyonayo ni muhimu sana katika Taifa letu, na amani inakuwepo tu kama watu watatendewa haki ndani ya Taifa. Haki hiyo ya kwanza ni ya kusikilizwa ambayo ndiyo hii mnayoifanya; Serikali tusikilizeni. Nikisema hapa, mimi sisemi ya familia yangu, ninasema ya Watanzania huko nje kwa sababu wamekosa fursa ya kuja kuingia ndani humu na kuyasema haya. Kwa hiyo, haki ya kwanza, Watanzania tunahitaji kusikilizwa yale tunayoyasema ili ninyi muweze kuyachakata na kuona ni namna gani mnakwenda kuyafanyia kazi kwa maslahi mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoamua kuwa wasikivu, tukawa na yale maneno ya kusema Serikali sikivu ya mdomoni kwenye moyo haipo, hatutalisaidia Taifa. Kwa sababu hata wawekezaji tunaowategemea, wakiona Serikali yetu inasema bila kutekeleza kwa vitendo, bado watakuwa na hofu na sintofahamu kwamba nikienda pale nitaenda kufanya nini? Kwa sababu Taifa lao lenyewe halina uhakika, watu wao wana vinyongo ndani ya nafsi. Kwa hiyo, naomba amani na suala zima la kusikilizwa lilindwe na lifanywe kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo, nakushukuru kwa muda, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nami kwa kunipatia wasaa niweze kutoa mchango wangu kwenye Bajeti Kuu ya Serikali ya 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la sekta ya uzalishaji na nitaomba nianze na Sekta ya Kilimo; kwenye Sekta ya Kilimo nitazungumuzia uzalishaji wa zao la mafuta ya kula ya alizeti. Mwaka 2021 Serikali ilikuja na mpango mkakati mzuri sana wa kwenda kupunguza ama kuondoa kabisa gharama kubwa tunayoitumia kama nchi ya kuagiza mafuta ya kula kutoka nje. Ikatuletea wananchi mpango wa kwenda kuzalisha zao la alizeti na ikateua mikoa mitatu ya kimkakati ili wananchi wa mikoa hiyo waweze kuzalisha kwa wingi ili tuweze kuona ni namna gani tunakwenda kuondokana na wimbi kubwa la upungufu wa mafuta ya kula ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia iliingia gharama ya kuhakikisha inawapatia wakulima mbegu ambazo zitakwenda kuwasaidia kuzalisha zao hili. Hata hivyo, pamoja na dhamira hii njema ambayo awali ilioneshwa na Serikali, lakini kwa sasa naanza kuiona Serikali ikirudi nyuma kwenye dhamira hii njema waliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema mwaka 2022, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa mafuta ya kula aliweka tozo ya asilimia 35, leo anakwenda kupunguza unaweka asilimia 25. Mheshimiwa Waziri, anachokitaka kukipata hapa ni nini? Leo wakulima wa alizeti wa Mkoa wa Singida, Mkoa wa Dodoma na Mkoa wa Simiyu tuna alizeti ya tangu mwaka 2022 ipo, mwaka 2023 tumeanza kuvuna, alizeti iko majumbani mwa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali wameamua kupunguza kodi kwenye mafuta ya kula, wazalishaji ama wachakataji wa zao la alizeti wamefunga viwanda, wameamua kuagiza mafuta, wanauza mafuta ambayo yanatoka nje na yana gharama nafuu, ambayo hawatumii umeme na wameondoa wafanyakazi kwenye viwanda. Mwisho wa siku, changamoto tuliyokuwa tunataka kuondokana nayo ya kupunguza wimbi la uingizaji wa mafuta ndani ya nchi tunakwenda kurudi kule kule tulikotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mwananchi waliyempa imani kwamba alime zao la alizeti inayojenga uchumi wa kwake binafsi…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Cosato Chumi.

TAARIFA

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Kunti kwamba, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 50, katika kuhakikisha kwamba tutakuwa hatupungukiwi na dola, mojawapo ya mikakati ni kuongeza uzalishaji ili kuongeza mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi. Sasa, kwa hili analolisema Mheshimiwa Kunti, maana yake badala ya kuuza nje sisi sasa tunataka tuagize nje zaidi kitu ambacho kama Serikali tutaji–contradict. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Kunti, unapokea taarifa?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono 36. Serikali wakati mwingine wanatuchanganya Watanzania. Leo ninavyozungumza hapa mwaka 2022 gunia la alizeti ni shilingi 27,000 na mwaka 2023 wananiambia ni shilingi 20,000 mpaka shilingi 25,000. Hivi ni mkulima gani tena atalala aote ndoto mwakani aende akalime alizeti? Hivi ni kweli Serikali ndio dhamira yao kwamba tunakwenda kuondokana na hilo wimbi kubwa la uagizaji wa mafuta ndani ya nchi? Mbona tunarudi kule kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri ili tuweze kufikia hilo lengo hii asilimia 25 aliyoiweka tunaomba aiondoe, tena hata hiyo asilimia 35 aliyokuwa ameiweka, safari hii nilikuwa nimekuja aweke asilimia 50 ili wawekezaji wa viwanda vyetu vya hapa ndani waweze kuchukua malighafi zilizoko ndani hapa ili waone akiagiza nje na akichukua za ndani ni heri achukue ndani kuliko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, sio zao la alizeti peke yake, tuna zao la mchikichi ambalo Serikali pia walifanya mkakati, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikwenda Kigoma kuzindua zao la chikichi, wakulima wa Kigoma leo wamelima michikichi, Serikali inaendelea kuondoa kodi kwenye mafuta, wanachotaka ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, achana na mchikichi, tuna pamba. Mimi nimeishi Mwanza, tulikuwa tunatumia mafuta ya pamba, leo mafuta ya pamba hayajulikani yalikofia ni wapi, wakati mbegu za pamba zipo na wakulima Mwanza wanalima pamba? Kwa hiyo, niishauri Serikali Wizara ya Fedha na Wizara za kisekta kwa maana ya Wizara ya Kilimo, waende wakutane wazungumze pamoja wawe kitu kimoja ili wanapokuja hapa wawe wanazungumza lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri wa Kilimo anahamasisha watu huko kulima mazao ya kuzalisha mafuta, Waziri wa Fedha anakwenda kuondoa tozo kwenye mafuta. Sasa ni kitu gani hiki wanachofanya? Wanatuchanganya, hatuwaelewi shida yao ni nini? Wazungumze, waje wakiwa na kauli moja ili tuweze kuokoa Taifa letu kwenye suala zima la uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie suala zima la mbolea kwenye Sekta hiyo ya Kilimo. Msimu uliopita mbolea ya kupandia ilichelewa sana katika maeneo mengi. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, tunaomba mwaka huu fedha itolewe mapema, mbolea ya kupandia ifike mapema ili wakulima wetu waweze kuondokana na adha kubwa ya kuchelewa kulima bila mbolea. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti kuna taarifa kutoka kwa Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Mwigulu.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri ambao Mheshimiwa Mbunge anachangia na Wabunge wengine wamechangia, nataka nitoe taarifa kwamba, tunapokea maoni yanayotuelekeza tupandishe kodi, lakini nilichotaka kutoa taarifa ni kwamba sio kwamba tumeshusha. Kwenye mafuta tumebakiza kodi iliyokuwepo mwaka 2022, kwa maana hiyo kwa kuwa maoni ya Wabunge tupandishe sisi tunalipokea hilo. Hata hivyo, tulibakiza kama ilivyokuwa mwaka 2022 kwa ajili ya kukabiliana na gharama za maisha. Kwa hiyo, kwa kuwa maoni ni kwamba tupandishe tumelipokea, lakini sio kwamba tumeshusha. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Kunti, unaipokea taarifa?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba azingatie hilo. Ni kweli apandishe ili viwanda vyetu nchini viweze kufanya kazi, kodi iweze kulipwa hapa ndani ya nchi ili vijana wetu na Watanzania wenzetu waweze kupata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nazungumzia suala la mbolea. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri, fedha itoke mapema ili tuweze kuagiza mbolea, iletwe wakati wa msimu wa kupandia kwa ile mikoa inayopanda mapema, waweze kupata mbolea ya kupandia kuliko misimu hii ya nyuma iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie pia tozo ya shilingi 100 kwenye lita ya petrol panoja na diesel. Tuna kama miezi kadhaa huku nyuma ambapo Serikali iliamua kuweka ruzuku kwenye mafuta diesel pamoja na petrol kutokana na wimbi kubwa la Vita ya Ukraine. Mheshimiwa Waziri, sasa naona hapa ametuletea ongezeko la tozo ya shilingi 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kuwa unapoongeza kodi kwenye mafuta ya diesel na petrol unapandisha nauli za usafiri, lakini gharama za vyakula pia zitapanda na kila kitu nchini kitapanda. Sasa namuuliza Mheshimiwa Waziri, hivi ni kweli tumekosa vyanzo vingine vyote vilivyopo mpaka twende tena kwenye mafuta ambayo miezi michache huko nyuma tumeweka zaidi ya shilingi bilioni nne kwa ajili ya kwenda kupunguza makali ya maisha kwa wananchi wetu? Hiki kitu anachokifanya Waziri hapa kinakwenda kuleta maisha magumu zaidi kwa wananchi wetu kwa sababu kila kitu kitapanda kutokana na suala zima la ongezeko la mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa haraka haraka dakika zangu zinakwenda. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna kodi ya shilingi 1,000 kwenye mfuko wa cement. Ujenzi ni gharama kubwa sana, bati gharama, nondo gharama, mchanga gharama, leo tena na cement wanaendelea kuongeza. Mheshimiwa Mwigulu, hahitaji wananchi wake wa pale Iramba wenye nyumba za udongo full suit chini na juu waweze kuwa na nyumba zenye matofari mazuri ya block waweze kuishi kwenye maisha mazuri anakwenda kuongeza tena kodi kwenye cement, kwenye nondo huku hapakamatiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe kama alivyoridhia kwenye suala zima la tozo ya mafuta, halikadhalika kwenye hili suala la tozo ya cement ya shilingi 1,000 kwa kila mfuko aende akaiondoe ili cement iweze kushuka na tuweze kupata nyumba bora kwa Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunti, ahsante sana muda wako umekwisha, nakushukuru sana.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, lakini nitumie fursa hii kukupongeza kwa nafasi uliyonayo. Hongera na naamini utakitendea haki kiti hicho. Naomba nianze kuchangia Wizara hii alipoishia Mheshimiwa Olelekaita kwenye migogoro ya hifadhi na watumiaji wengine wa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Mkoa wa Dodoma tuna mapori mawili ambayo yako Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa. Pori la Mkungunero ambalo lipo Kondoa na Pori la Swagaswaga ambalo lipo Wilaya ya Chemba. Pori hili la Mkungunero limekuwa ni kichaka cha Maafisa wa Wanyamapori kutesa Watanzania wasiokuwa na hatia eti kwa sababu tu wana ng’ombe, eti kwa sababu tu ni wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2019 nilizungumza ndani ya Bunge hili nikaeleza mateso na manyanyaso wanayopata wananchi wa wilaya ya Kondoa kwa Kata ya Keikei, Kata ya Kinyasi pamoja na Kata ya Itasu. Mheshimiwa Waziri nimekuja kwako mara kadhaa nikiwa nakulalamikia suala hili na ninyi Wizara mnasema kuna shida gani? Pale tumemaliza kabisa Mkungunero. Ukweli ni kwamba mnafukia kombe mwanaharamu apite wakati Watanzania wanaumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki mbili zilizopita kuna wananchi watatu ambao wamekamatiwa ng’ombe wao. Wawili wamelipa kwa makubaliano na Maafisa Pori wa Hifadhi ya Mkungunero. Mmoja akakataa akapelekwa Mahakamani, ng’ombe 50 kalipa shilingi milioni 10 faini. Hivi huyo mwananchi mkulima, mfugaji anayetegemea mifugo yake kwa ajili ya kuendesha maisha yake ya kila siku na kulichangia kodi Taifa hili, mnachomtafuta ni nini watu wa hifadhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi, katika hifadhi ile kuna akina mama ambao wanafanya shughuli zao mbalimbali za kujitafutia uchumi, wamekuwa wakibakwa kwenye Hifadhi ya Mkungunero, wamekuwa wakipata mateso ya kurushwa kichurachura, kupigwa na kila aina ya mateso kadha wa kadha wanayoyapata kwa ajili ya hilo pori. Mheshimiwa Waziri, kuna shida gani? Serikali ni moja, chama kimoja, Mawaziri mnakaa kwenye Baraza la Mawaziri, mnashindwaje kukaa chini na kuweza kutatua mgogoro wa pori hili? Serikali Sikivu, Serikali ya wanyonge mnaotamani kuwapigania Watanzania, hawa Watanzania hawana hatia, ardhi haiongezeki Mheshimiwa Waziri, watu tunaongezeka.

Pori lile Mheshimiwa Waziri kwa akili tu ya kawaida, Warangi sisi hatuna mahali pa kwenda. Lile ndiyo eneo letu tumezaliwa kule, twende wapi? Tunaomba Pori ya Mkungunero, kagaweni eneo, tuachieni na sisi watoto na wajukuu tuendelee kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pori la Swagaswaga Wilaya ya Chemba Kata ya Lahoda, pale kuna wafugaji; na ninashukuru Mheshimiwa Mpina amelisema. Kuna wafugaji mwaka 2018/2019, Mheshimiwa Mpina ukiwa Waziri wa Mifugo, Mheshimiwa Ulega akiwa Naibu Waziri wako; Mheshimiwa Ulega alienda Wilaya ya Chemba Pori la Swagaswaga akakutana na wafugaji waliokamatiwa ng’ombe wao wasiokuwa na hatia wamewekwa pale, hawana chakula, hawana maji, hawana dawa, hawana chochote. Ng’ombe wamekufa zaidi ya 500. Tulisema humu ndani, hamkutaka kusikia eti tu kwa sababu mnalinda uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji uhifadhi lakini siyo kwa maisha ya mateso ya namna hii mnayotufanyia Watanzania. Mkitushirikisha wananchi, tutaulinda huo uhifadhi kwa sababu na sisi tunautaka na tunauhitaji sana. Ila kama mtaendelea kutunyanyasa, kututesa na kutuonea, hata hao wahifadhi wenu mnaowaleta kule, ipo siku hapatatosha. Tutachoka kunyanyaswa, tutaamua kuchukua hatua mkononi, kitu ambacho sitamani kitokee. Mheshimiwa Aida amesema, kwake imeshatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mstaafu Mheshimiwa Mpina kasema. Zaidi ya ng’ombe 400 mpaka leo Wizara ya Maliasili hamtaki kurudisha ng’ombe wale, mnachotaka ni nini? Mmewapeleka wapi hao ng’ombe? Nani anao mpaka leo miaka miwili?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa mchango wangu kwenye itifaki hii. Kwanza nawapongeza Serikali kwa kuona sasa ni wakati umefika wa kuweza kutuletea azimio hili au itifaki hii. Itifaki hii ina maslahi mapana sana na wakulima wetu pamoja na wafugaji. Pale wafugaji na wakulima wanaponufaika ni moja kwa moja Taifa letu linakwenda kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kwenye mambo kadhaa ili tuweze kufanya vizuri. La kwanza, kwenye itifaki hii, kwenye suala zima la mifugo, afya ya mimea pamoja na mazao yote, tuna upungufu mkubwa wa wagani ambao wao ndio wana uwezo wa kwenda kuhakikisha bidhaa zetu kwa maana ya mifugo yetu, mimea yetu, matunda yetu, mboga zetu na kila kitu itakwenda kukidhi mahitaji ya itifaki hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kumekuwa na kigugumizi cha muda mrefu cha kutokuajiri Maafisa Ugani. Sasa naiomba Serikali, kwa kuwa tumeamua kuingia kwenye itifaki hii, ni wajibu wetu kama nchi kuona umuhimu wa kwenda kuajiri Maafisa Ugani wa kutosha ili tuweze kunufaika na hii itifaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ni suala zima la watafiti. Bila utafiti pia bado hatutaenda kuleta tija kwenye hii itifaki. Watafiti wetu wametengwa, wametelekezwa, hawana chochote ambacho wanakifanya. Wapo tu wanaitwa watafiti, lakini kwa maana sasa ya kwenda kutekeleza na kupata tija kwenye itifaki, naomba Serikali ione namna bora ya kwenda kuwaongezea fedha za kutosha watafiti wetu ili waweze kufanya kazi nzuri itakayoleta matunda kwa Taifa letu kwa ajili ya hii itifaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamesema suala zima la wadhibiti ubora; na Mheshimiwa Ndakidemi amesema kwamba TBS imezidiwa, ni kweli. Sasa wakati Serikali inakwenda kuangalia ni namna gani ya kuanzisha chombo kingine ambacho kitakwenda kumsaidia TBS, naiomba Serikali iende ikaongeze nguvu ya bajeti, pamoja na wataalam na vitendea kazi TBS ili waweze kuifanya hii kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, kuna suala zima la elimu kwa watendaji wetu ambao wako mipakani. Pia naomba nchi wanachama tukiwemo sisi Watanzania, twende tukatoe elimu kwa watendaji wetu ambao wako mipakani ili waweze kuelewa mkataba huu ni namna gani ulivyoingia? Ni vitu gani vinavyozingatiwa? Ubora ni upi? Hii itaondoa changamoto kwa Watanzania wetu ambao watakwenda kufanya hizo biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo natamani pia kuishauri Serikali, ni kuona sasa itifaki hii inaenda kuwa ni mwarobaini wa changamoto mbalimbali zinazotokana na upungufu wa bidhaa zetu tunapokwenda kuzipeleka kwao ama zinapokuja kwetu. Tuliona miaka michache iliyopita, miwili au mitatu, tuliteketeza vifaranga, lakini tuliona mahindi yetu yakikataliwa mpakani. Sasa kwa mujibu wa hii itifaki, iende ikatuweka wamoja na tutafute njia mbadala nzuri itakayokwenda kutusaidia kuondokana na hizi changamoto za kuwa tunaendelea kunyoosheana vidole na nchi za wenzetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kwa msisitizo tu ni suala zima la sheria kwamba Wizara sasa mtuletee Muswada wa Sheria, Kanuni na Sera ili tuweze kupata kitu kitakachokwenda kutusaidia kuisimamia itifaki hii. Msipotuletea mapema, ina maana tutaidhinisha leo, then tutaenda kuweka makabatini kwenye shelves zetu, hatutaweza kufanya kitu chochote na mwisho wa siku itakuwa hakuna kitu chochote kinachokwenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru kwa nafasi. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye hizi Kamati zetu mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunakubaliana kwamba bila kilimo sisi sote humu tusingekuwepo ndani, kwa sababu tunakula chakula ili tuweze kupata afya bora na akili timamu kwa ajili ya kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani, kumbe cheo kimebadilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye mtiririko wa utoaji fedha kwa Wizara ya Kilimo, Wizara ya Kilimo bado iko chini, Wizara ya Kilimo bado inaendelea kusahaulika, Wizara ya Kilimo bado imetupwa kabisa huko mafichoni ilhali hii Wizara hii ndio tunayoitegemea Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania zaidi ya 65% ndio wanapata ajira kupitia Wizara hii. Inatulisha na inatoa ajira, lakini Wizara hii ndiyo inayohangaika wakulima wake ambao ni zaidi ya 80% huko vijijini watafute mbegu wenyewe, watafute pembejeo za kilimo wenyewe, mvua wanategemea ya Mwenyezi Mungu, kilimo cha kudra ya Mwenyezi Mungu, lakini Wizara hii Serikali haijawahi kuonesha nia na dhamira ya dhati ya kuisaidia ili tuweze kuliokoa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Mfuko wa Pembejeo wa Taifa; Mfuko huu pamoja na Benki ya Kilimo, nianze na Mfuko wa Pembejeo wa Taifa; mfuko huu wa pembejeo wa Taifa tulitegemea Serikali itoe feddha za maendeleo kwenye Wizara ili huu Mfuko wa Pembejeo wa Taifa waweze kupatiwa fedha ili wakulima wetu wadogo wadogo kule chini waweze kupata zana za kilimo na waweze kulima kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Wizara imekuwa ikinyimwa fedha na mfuko huu umeendelea kukosa fedha, matokeo yake mfuko uko pale, watumishi wako pale, hakuna kazi yoyote wanayoifanya; wanaamka asubuhi wanakuja wanasaini, wanapumzika wanasubiri muda ufike warudi majumbani kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali inaona kilimo hakina tija kwenye Taifa hili niombe tuifute hii Wizara ili wakulima wa nchi hii tuendelee kulima kwa namna tunavyoweza kuliko kuwa na Wizara ambayo haina msaada kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, Benki ya Kilimo; benki hii tumeendelea kuipigia kelele humu ndani, kila siku story ni zile zile, maneno ni yale yale na imebadilika sasa mmebakisha kufukuza kila siku mnatubadilishia Wakurugenzi; sasa huyu Mkurugenzi haujampatia fedha, unamfukuza, ulitaka afanye nini? Si amekaa tu, fedha hakuna, atamkopesha nini huyo mkulima? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niiombe sana Serikali; kama kweli tuna nia na dhamira ya dhati ya kuinua kilimo cha Taifa hili na kujenga uchumi wa nchi hii, twendeni tukaongeze fedha kwenye Wizara ya Kilimo ili tuweze kuleta tija katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji; Wizara ya Maji angalau safari hii imepata mkongojo imesogea, lakini changamoto kubwa iliyoko Wizara ya Maji ni miradi mikubwa ya kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu nikiwa nje huko sijaingia kwenye jengo hili kulikuwa na mradi unaitwa Mradi wa Bwawa la Kidunda, una zaidi ya miaka 20 leo Bwawa la Kidunda halijakamilika. Sasa sijui shida ni nini kwa Serikali kwenda kutekeleza miradi hii mikubwa ambayo ina tija kubwa kwa Taifa letu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa natamani sana, tunaitaka Serikali na tumeendelea kuwashauri Wizara pamoja na Serikali, kwa maana ya Wizara ya Fedha, watusaidie hii mikataba wanayoingia na wafadhili kama wanaona haiwezekani hao wafadhili waliokuja wawaondoe watafute wafadhili wengine ili miradi iweze kutekelezeka. Napata hofu sana, Mkoa wa Dodoma leo tuna Mradi wa Farkwa, sasa hivi una zaidi ya miaka sita tunakwenda was aba, tumelipa fidia, lakini suala ni lini tunaanza ujenzi wa Bwawa la Farkwa? Story, kwa hiyo, tukakwenda humu ndani, watakuja, watakuja, watakuja; bado hatujakamilisha mazungumzo, bado watu sijui wanafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maneno yamekuwa ni mengi kuliko utekelezaji na uchukuaji wa maamuzi. Serikali tunaiomba iwe inafanya haraka kwenye suala zima la uchukuaji wa maamuzi ili kupunguza muda wa kuendelea kupoteza mud ana kutokutekeleza miradi hii kwa wakati. Nakushukuru, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia wasaa na mimi wa kuweza kutoa mchango wangu kwenye hizi Kamati zetu mbili, USEMI, lakini na Huduma. Ninawashukuru na niwapongeze Kamati kwa kazi kubwa waliyoifanya, hususan Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuwasemea wana-Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, wakati tunapata uhuru ardhi ya Manispaa ya Dodoma au ya Halmashauri wakati huo ya Dodoma ilikuwa chini ya wana-Dodoma, lakini mnamo mwaka 1973 Serikali ikaamua kuiweka ardhi yetu chini ya Ustawishaji wa Makao Makuu (CDA), ili Dodoma kama Makao Makuu ya nchi iweze kupangwa na kupangika ili ifafane na miji mingine duniani.

Mheshimiwa Spika, CDA ikaishi takribani miaka 43 kuanzia mwaka 1973 mpaka 2016 ambapo Hayati Rais John Pombe Magufuli aliamua kuivunja CDA. Ilivunjwa kwa sababu CDA hawakuweza kufanya kazi ya kupanga Mji badala yake walikuwa ni chanzo cha migogoro kwa wana-Dodoma. Tukaivunja, ikavunjwa CDA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matarajio ya wananchi wa Dodoma yalikuwa baada ya kuondolewa CDA ardhi yao imerudi Halmashauri kwamba, wana-Dodoma sasa watakwenda kumiliki ardhi yao na migogoro itakwenda kuisha. Kwa bahati mbaya sana hivi tunavyozungumza wananchi leo wa Dodoma wanasema ni afadhali ya CDA kuliko ardhi ilivyorudi kwenye Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, hawa Watumishi baadhi baada ya CDA kuvunjwa, baadhi walipelekwa kwenye Halmashauri zingine, baadhi wamebaki ndani ya Jiji la Dodoma kwenye kitengo cha ardhi. Mkurugenzi leo wa Dodoma ndiye aliyekuwa Afisa Mipango ndani ya CDA. Leo ni Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, anafahamu vizuri suala la mgogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tuna hati wananchi kiwanja kimoja kina hati zaidi ya tatu. Wale wenye fedha wenye mabavu ndiyo wanaoweza kumiliki ardhi leo kwenye Jiji la Dodoma, wale wanyonge hawawezi kumiliki ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu, kwenye ushirikishwaji wa upangaji ama wa upimaji wa ardhi, makubaliano yalikuwa ardhi yako ukionesha unatoa asimilia 10 kwa ajili ya barabara, asilimia 30 wanachukua Jiji, asilimia 70 unapewa mwananchi, haifanyiki hivyo. Wale wengine ambao wana viwanja vidogovidogo wanaunganishwa hapo baadae wakija kuhoji viwanja vyao viko wapi wanaambiwa kimeliwa na barabara, kwa hiyo huna kiwanja. Hayo ni mateso wanayopitia watu wa Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, hiki kitu iinaumiza sana. Tuna wajane, tuna wagane, tuna watoto yatima wako hapa ambao leo wananyimwa ardhi yao kwa sababu ya Watanzania wenzetu ambao tumewapa nafasi, waweze kuwasaidia na wao watoke kwenye wimbi la umaskini walilonalo, wao wako wanaatamia ile ardhi, wanaitumia wanavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati imesema kwamba, watu wachukuliwe hatua kuhusiana na suala zima la migogoro ya ardhi ya Dodoma. Naomba niongezee, hawa watu ambao walikuwepo tangu CDA na mpaka leo bado wako pale ofisini wapaki magari yao pembeni, uchunguzi upite, wakiwa wao wako pembeni, ili tujue shida iko wapi Dodoma, kwa nini Dodoma na siyo sehemu nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nihame kwenye suala zima la Dodoma, naomba niende kwenye suala zima la elimu. Tunashukuru Serikali kwa kutuongezea madarasa kwenye shule zetu mbalimbali, lakini wakati tunaomba haya madarasa wakati mwingine na sisi huku vijijini ama kwenye maeneo yetu tunakuwa tunaendelea kuwaza tufanye nini ili watoto wetu waweze kupata elimu yenye mazingira rafiki.

Mheshimiwa Spika, tunayo changamoto moja Halmashauri ya Wilaya ya Chemba. Tulipewa Shilingi Milioni 140 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa Saba shule ya Sekondari Mrijo. Kata ya Mrijo ina Vijiji Saba, Vijiji Vitatu mwanafunzi anatakiwa kutembea zaidi ya kilometa 60 kwenda na kurudi. Wananchi wakaamua kujihamasisha waweze kutoa Kijiji ambacho kipo katikati wajenge, waanzishe pale shule ili waweze kujenga shule nyingine ya sekondari, waache shule mama ya Mrijo waje wajenge shule nyingine pacha ya Mrijo ambayo itakuwa inaitwa Mrijo Juu.

Mheshimiwa Spika, sasa tukawaomba na wananchi wakajitolea, wamefyatua tofali, wamesomba mchanga, wamesomba…

SPIKA: Sekunde 30, malizia.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, tukawaomba Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa haya madarasa saba badala ya kupelekwa pale Mrijo Chini ambako tuna madarasa 24 tunaomba tuyalete huku Mrijo Juu ili wanafunzi wetu ambao wanatembea zaidi ya kilometa 60 kwenda na kurudi tuwapunguzie huo umbali ili waweze kusoma katika mazingira rafiki, lakini Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa hawajaweza kutuelewa hilo. Kwa hiyo, niombe sana hebu watuone kwenye jicho hilo, kutembea kilometa 60 ni mtoto wa Mbunge gani anayeweza kutembea kilometa 60 kwenda na kurudi halafu sisi tunawanyima wananchi wetu kwa kodi zao wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwenye suala hili waweze kuliangalia vizuri. Nakushukuru kwa wakati. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kutoa mchango wangu kwenye sekta hii muhimu ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya na uhai.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri, nina uzoefu wa miaka sita, sasa tunakwenda saba; kwenye Wizara hii ya Kilimo kila Waziri anayekuja amekuwa na maneno matamu sana ya kutupa matumaini makubwa wakulima wa nchi hii. Sijawahi kuwa na shida na matumaini ya maneno matamu ya kumtoa nyoka pangoni. Shida yangu kubwa Mheshimiwa Bashe ambalo mpaka sasa kwa hotuba yako tamu uliyoitoa leo kulihutubia Taifa hili: Je, haya uliyotunenea mbele ya Bunge hili, Mheshimiwa Mwijage amesema umelihutubia Taifa; ndiyo na kweli umelihutubia Taifa, yatakwenda kutekelezeka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya unayoyasema, yasemwa miaka nenda, miaka rudi, lakini hatujawaji kuona utekelezaji wake. Suala la bajeti tulisema sana, lakini mkawa mnaongezewa, mnaongezewa, mnaongezewa. Shida siyo kuongezewa bajeti kwenye vitabu, shida ni utolewaji wa fedha kwenda kwenye utekelezaji wa miradi. Wakati mwingine nikikuangalia nakuonea huruma kama vile unaanza kuzeeka kabla ya umri wako, lakini ndiyo hivyo tena tumekupa majukumu, kubali kuzeeka. Utalitendea haki Taifa hili kama haya uliyoyanena leo kulihutubia Taifa hili, utakwenda kuyasimamia kwa dhati ya moyo wako wakulima wa nchi hii wakaona uwepo wako kwenye hii Wizara. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba maneno yake ni mazuri na tunaona njia na nuru ya bajeti yake, lakini Mheshimiwa Waziri huwezi ukawa na miujiza yoyote yakutekeleza haya kama hutakuwa na wasaidizi wa kutosha kwenye Wizara yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee tu mfano upungufu wa watumishi kwenye Chuo Kikuu cha Sokoine. Chuo hiki ndicho kinachotuzalishia wataalam; na watalaam hao ndio tunawategemea watoke chuoni waende field kwa wananchi wetu kule kusaidia kilimo bora, kilimo chenye tija kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhitaji wa watumishi Chuo Kikuu ni 2,076; tulionao ni 1,253. Tuna upungufu wa zaidi ya watumishi 800. Bila ya hawa kuwepo, haya yote aliyoyaeleza Mheshimiwa Waziri itakuwa ni kazi bure. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Bashe, tunakuomba usimame kwenye ajira zinazokuja hizo zilizotangazwa na naiomba Serikali, kipaumbele iwe ni sekta ya kilimo tupate watumishi wa kutosha waende wakatusaidie kwenye suala zima la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la pili ambalo natamani kulisema leo, ni suala zima la ushirika. Wote tunaamini kwenye suala zima la ushirika, lakini nina changamoto moja. Moja ameisema kaka yangu Mheshimiwa wa Jimbo la Kishapu kuhusu upungufu wa watumishi, lakini pamoja na upungufu wa watumishi wa Ushirika, halikadhalika watumishi waliopo baadhi yao sio waadilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna madhaifu makubwa sana ya watumishi wa Kitengo cha Ushirika kutokuwa waadilifu, lakini kwenye ushirika huko huko watumishi wetu, Maafisa Ushirika, wao ndio wanajifanya wamiliki wa ule ushirika ilhali wamiliki wa ushirika ni wananchi wenyewe walioamua kujiunga kwenye ushirika, lakini wao ndio wamekuwa ma-top wa ule ushirika kiasi kwamba kupelekea watu na Watanzania kuuchukia ushirika kwa sababu ya watumishi wasiokuwa waadilifu kwenye sekta ya ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike? Namwomba Mheshimiwa Waziri, watumishi wote wa sekta yako ya ushirika ambao sio waadilifu, suluhisho lisiwe kumtoa Chemba kumpeka Hombolo, suluhisho ni apaki gari lake pembeni hili atupishe tuweze kufanya kazi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilitembelea Mikoa ya Kusini kwa ajili ya kwenda kuona namna gani ushirika unafanya kazi. Tumekuta watu kule wako vizuri na mfumo wao uko vizuri; na leo kwa mara ya kwanza nakuwa muumini wa Stakabadhi Ghalani ambayo niliipinga kikao kilichopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofika kule nikakuta watu hawa kwenye ushirika wao wanafanya mazao yao vizuri, wanauza mazao yao vizuri, na kiasi kwamba inapelekea kwenda kuwa na vitega uchumi ambavyo vina fedha nyingi sana. Ila changamoto iliyopo, watu hawa unakuta wanamiliki mradi wa Shilingi bilioni 1.5 lakini watu hawa wanakwenda kukopa fedha kwa ajili ya kumpeleka mtoto wake shule, analipa riba ya asilimia 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri, naomba ushirika uende ukawafundishe wananchi wetu ambao wako tayari kujiunga na ushirika namna ya kujiwekea akiba kwenye vyama vyao badala ya kwenda kukopa benki, waepukane na kodi ya asilimia 24 waweze kuchukuwa fedha yao ile iliyoko pale waweze kukidhi mahitaji yao wakiwa wamevuna mazao yao na wanasubiri msimu wao wa bei kupanda ili waweze kuvuna mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba pia nizungumzie suala zima la kodi kwenye zana za kilimo. Tuna changamoto kubwa sana kwenye zana zetu za kilimo na hili limesemwa hapa. Tuna mfuko wa pembejeo ambao sasa unaenda kuzama baharini. Sasa hebu fikiria, leo mwananchi wa kawaida, wa Itololo kule ambaye ana eka zake tano au kumi, anatamani kutoka kwenye kilimo cha jembe la mkono angalau akanunue power tiller ama hata trekta, lakini ukienda kuuliza bei ya power tiller ni shilingi milioni kumi na kitu, shilingi milioni saba, na kadhalika; ukigusa trekta, shilingi milioni 45, shilingi milioni 60, shilingi milioni 30. Ni mwananchi gani wa nchi hii jamani anayeweza kumiliki trekta kwa bei hizo?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuondokana na kilimo kisichokuwa na tija na tuwasadie wakulima wetu, tunaiomba na Serikali kwa ujumla, zana za kilimo.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: … wananchi waweze kumiliki matrekta na kuleta tija kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa mara nyingine tena. Nasimama kwa masikitiko makubwa sana kwenye Wizara hii ya Ujenzi. Kwa bahati mbaya sana Mheshimiwa Waziri aliyepo leo ndiye aliyekuwepo Bunge lililopita, Bunge la Kumi na Moja, nikipoingia humu ndani. Katika Ubunge wangu wa miaka saba sasa nakwenda, kila nikisimama kwenye Wizara hii naisema barabara ya kutoka Kibirashi mpaka Kwa Mtoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii mwaka jana kwa mara ya mwisho walituambia wametenga kilometa 50, lakini kwa kuanza wanakwenda kuanza na kilometa 20 na nikawaambia kwa nini kilometa 20 na zisiwe kilometa 50? Cha ajabu walichokwenda kukifanya ndani ya mwaka mzima tuliowapitishia bajeti ya kwenda kutekeleza miradi ya maendeleo kwa Watanzania, walichoenda kufanya kwenye Barabara ya Kibirashi mpaka Kwa Mtoro, wamesaini mkataba wa kwenda kuanza kazi, mwaka mzima wanasaini mkataba. Hii barabara nilishasema humu ndani, ina ahadi ya Mheshimiwa Hayati Mkapa, ahadi ya Mheshimiwa Kikwete na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020 na 2020 – 2025 sasa, lakini barabara hii kila siku wanatupa hadithi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakienda na staili ya kilometa 20, barabara hii ina takribani kilometa 460, Serikali ya Chama cha Mapinduzi ili iweze kukamilisha barabara hii inahitaji miaka 23. Hiyo miaka 23 wanayoihitaji, ni kama kila mwaka watajenga hizo kilometa 20, lakini kwa kuwa wanatumia mwaka mmoja kusaini mkataba wa kujenga kilometa 20 wanahitaji miaka 46 ili waweze kuikamilisha hii barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa barabara na ukubwa wa Taifa hili, barabara tu ya kilometa 460 wanahitaji miaka 46, nashindwa kutafakari, yaani nashindwa kuelewa kwenye suala zima la hii barabara. Nilishasema hapa kwamba, kama Serikali inaona barabara hii sio kipaumbele na haina tija kwa Watanzania wa Mikoa minne, Tanga, Manyara, Dodoma na Singida, waifute tujue hatuna barabara kuliko kuwa wanatuandikia kwenye barabara kila mwaka. Barabara inakuja ina maandishi, wanatenga fedha halafu hawaendi kutekeleza, wakija wanatupa maandishi, watuondoe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachosema hiki wakati mwingine tunaumia, kwa sababu Waheshimiwa Wabunge hapa wamesema, kuna watu wanabandua lami wanabandika lami. Sisi Mkoa wa Dodoma ukiangalia maunganisho tuliyounganishwa, jimbo ambalo angalau lina barabara za kutosha za lami ni Jimbo la Dodoma Mjini, ukienda katika majimbo yote ya vijijini hatuna lami. Leo kwenye kilimo, Mkoa wa Dodoma ni mkoa ambao ndio unaokwenda kulima zao la alizeti na wilaya pekee kwa Mkoa wa Dodoma ambayo ndio inatekeleza kilimo cha mkakati cha zao la alizeti ili tuondokane na uhaba wa mafuta nchini ni Wilaya ya Chemba, lakini barabara yake haitengenezwi. Hiyo alizeti Watanzania wa Wilaya ya Chemba wakilima wanaifikishaje sokoni? Inafikaje sokoni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii, hizi kilometa 20 ambazo unaanzia Kibirashi, kama wameamua kuanza na kilometa 20 niombe, Mkoa wa Dodoma kuanzia Oloboroti pale twende na sisi wakatutengee kilometa 20, otherwise hatutaelewana na Mheshimiwa Waziri. Ameanza kilometa 20 Kiberashi ameshapanga wamesaini mkataba, twende akatutengee na sisi Chemba, Mkoa wa Dodoma, kuanzia Oloboroti mpaka Kwa Mtoro pale tumalizane salama, otherwise humu ndani leo, labda Kiti kininyime nafasi, la sivyo hatutaelewana. Uzuri ni yeye huyohuyo kwenye hii Wizara na kwenye hiyo barabara, wakija wanatoa tabasamu nzuri, wanaonesha sura za huruma, Watanzania wanaumia kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mto umepita pale Songoro, ule mto ni mkubwa haujawahi tokea. Watu wanakufa, watoto wa shule wanakufa katika mto ule wakati wa mvua masika; wao wako hapa wanafurahi kwa kuwa familia zao hazipati changamoto hizo ambazo Watanzania maskini kule chini wanazipitia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende katika suala zima la ulipaji wa fidia. Barabara hii wananchi wa Kata za Mrijo, Chandama, Songoro, Goima, mpaka Kwa Mtoro waliwazuia wananchi hao wasifanye maendelezo ya nyumba zao. Miaka 17 sasa hawajawalipa fidia, barabara hawajengi, Serikali ya watu maskini, wako wapi hao maskini? Mheshimiwa Waziri akija kuhitimisha hoja yake aniambie wanajenga barabara au hawajengi? Fidia wanalipa ama hawalipi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hawalipi fidia wawaruhusu wananchi wa Wilaya ya Chemba waendeleze viwanja vyao kuliko kuendelea kuwapotezea muda na kuwaweka kwenye umaskini ambao haukuwa ni hitaji lao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Uwanja wa Ndege wa Dodoma, Makole. Mwaka 2016 walikuwa wanafanya upanuzi wa uwanja wa ndege wakiwa wanasubiri kuanza ujenzi wa Uwanja wa Kimataifa wa Msalato. Mwezi wa Mei, 2016 wakawathaminisha watu nyumba zao kwamba, zinaondoka ili wafanye upanuzi. Tangu mwaka 2016 mpaka leo hawajalipa fidia za watu wa uwanja wa ndege, wamelipa baadhi wengine wamewaacha. Mheshimiwa Waziri akija kuhitimisha hapa aniambie fidia ya uwanja wa ndege pale analipa au halipi? Kama halipi, awaruhusu wananchi wa Kata ya Makole waendeleze nyumba zao, wafanye innovation za nyumba zao. Msiendelee kuwatia watu umaskini, umaskini sio sifa, wasitupotezee muda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja nimalizie. (Makofi)