Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Stanslaus Shing'oma Mabula (41 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kulikuwa na itilafu ya mitambo kidogo, naitwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Jimbo la Nyamagana. (Makofi/Vigelele)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ametupa fursa ya kuwepo hapa ndani, lakini nitumie nafasi hii pia kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Nyamagana kwa kufanya maamuzi sahihi kuwakataa watalii na kuleta wachapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maandiko matakatifu Hosea 4:6 inasema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Kwa hiyo, nataka nikuthibitishie maandiko haya yako watu yanawahusu moja kwa moja. Kwa hiyo, tuliobaki humu tusiwe na shaka kwa sababu sisi tuna maarifa, tunayo kazi ya kulitumika Taifa na Watanzania. Mara zote nimekuwa ninasema tumeanza na Mungu, tutamaliza na Mungu na ndivyo itakavyokuwa. (Makofi)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuchangia kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake iliyokuwa imejaa na kusheheni mahitaji ya Watanzania. Watanzania wengi wakati wote tumekuwa na subira lakini tumekaa tayari kutegemea hiki ambacho Mheshimiwa Rais sasa anakifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda moja kwa moja kwenye kuchangia hotuba hii yako masuala ya msingi ya kuzungumza juu ya Jimbo langu la Nyamagana lakini juu ya Taifa zima kwa ujumla. Nianze na sekta ya afya. Mheshimiwa Rais amezungumza sana juu ya kuanzisha zahanati kwenye kila kijiji, kituo cha afya kwenye kila Kata, lakini kuhakikisha kila Wilaya ina hospitali na Mkoa una hospitali ya rufaa na Kanda zinazo hospitali za rufaa kwa ajili ya kuhudumia Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo ninalotoka mimi la Nyamagana linazo hospitali 12 peke yake kwa maana ya zahanati, lakini siyo Nyamagana tu, ninaamini yako maeneo mengi sana. Kihalisia tunapozungumza kumhudumia mwananchi kwenye sekta ya afya, kuanzia ngazi ya Kijiji, ngazi ya Kata na ngazi ya Wilaya, tunapozungumza kuanzisha hospitali hizi ili zikamilike hospitali yako mambo mengi yanayohitajika, unazungumzia habari ya majengo, watumishi wenye nia njema na thabiti ya kuwatumikia Watanzania, unazungumzia vifaa tiba zikiwemo dawa ili kuhakikisha vyombo hivi na nyumba hizi zinapokuwa tayari Watanzania wenye matumaini na Serikali hii waweze kupata mahitaji yao, tukiamini afya ni suala msingi ambalo linaweza kuwa ni chombo peke yake kwa mwanadamu kinachomfanya awe na uhakika wa kupumua wakati anapopata matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini Nyamagana inabeba Hospitali ya Rufaa ya Bugando, hospitali hii ni kimbilio la wakazi zaidi ya milioni 14 wa Kanda ya Ziwa, lakini iko based kwenye Jimbo la Nyamagana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wanalalamikiwa sana, lakini inawezekana watumishi wanalalamikiwa sana sisi kama Serikali hatujafanya wajibu wetu. Niiombe Serikali ya Awamu ya Tano hospitali yenye vitanda zaidi ya 950 inayotegemewa na watu zaidi ya milioni 14 inaomba bajeti ya takribani bilioni saba kwa mwaka mpaka leo tuko zaidi ya miezi sita imepata milioni 106 peke yake, wananchi wataendelea kulalamika, watumishi wataonekana hawana maana kwa sababu hawatoi huduma zilizobora. Bili ya maji peke yake na umeme kwa mwezi ni zaidi ya milioni 60. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana tuangalie masuala haya kimsingi ili tuweze kutoa huduma. Nyamagana ni Jimbo peke yake lenye kilomita za mraba 256 kilomita 71 zikiwa ni maji lakini hatuna maji ya uhakika ya bomba kwa wananchi wa Jimbo la Nyamagana. Hili ni tatizo na lazima liangaliwe kwa undani. Liko suala la elimu limeshazungumza sana na mimi naunga mkono na wale waliolizungumza. (Makofi)
Suala la miundombinu pia limezungumzwa ziko barabara ambazo hazipitiki, Nyamagana Mheshimiwa Rais wakati amepita ameahidi kuimarisha barabara zinazosimamiwa na TANROAD na zile ambazo alifikiri kwa ahadi yake zitatekelezeka, kutoka Buhongwa kupitia Lwanima, Kata ya Sahwa, Kishiri kuunganisha na Igoma, Fumagira kuunganisha na Wilaya za Misungwi na Magu. Lakini kutoka Nyakato kupita Busweru kwenda Kabusungu, kwenda kutokea Bugombe, Igombe na kuunganisha na Kata nyingine, hii barabara ili iweze kupitika kwa mama yangu Mheshimiwa Angelina kwa sababu haya ni majibu pacha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la miundombinu naomba niseme kwamba liko tatizo kubwa, Serikali hii imejipambanua kukusanya mapato ni lazima tuhakikishe tunapata vyanzo vya mapato. Mwanza ni kituo kikubwa ambacho kinaunganisha mikoa ya Kanda ya Ziwa, nchi za Afrika Mashariki na Kati na Maziwa Makuu hakina airport ya maana ambayo inaweza kuongeza mapato kwa asilimia kubwa. Tuone umuhimu wa kujenga airport ya maana, Internation Airport ambayo itasaidia mtalii anayekwenda Ngorongoro kutokea Arusha akipita kule atokee Serengeti aje aondokee Mwanza, akishukukia Mwanza apite Serengeti aende Ngorongoro aondokee Arusha. Lakini bandari tunaunganisha mikoa zaidi ya sita hakuna bandari ya maana Mwanza hili na lenyewe liangaliwe kwa maana sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, juu ya ukusanyaji wa mapato. Nimuombe Waziri wa TAMISEMI, hakuna siku itakaa Halmashauri hizi ziweze kujitegemea asilimia 50 mpaka 100 maana yake ni kwamba uwezo huo ni mdogo sana lazima tujipange kukusanya mapato.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mabula muda wako umekwisha.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja asilimia mia. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia na mimi angalau kidogo na nitajikita zaidi kwenye viwanda vyetu katika Jiji letu la Mwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kupata fursa nyingine tena leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka miaka michache iliyopita Mji wa Mwanza ulikuwa maarufu sana kwa viwanda vya samaki na watu wake wengi sana walipata nafasi za maendeleo, za kiuchumi na uchumi kwa kweli ulikua sana. Hata asilimia tunayoizungumza leo inayochangiwa kwenye pato la Taifa na Mkoa wa Mwanza imetokana sana na imetengenezwa na viwanda vya samaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa viwanda hivi vya samaki leo ni viwanda ambavyo vinajiendesha kwa hali dhoofu sana. Nasema dhoofu sana kwa sababu zao hili la samaki miaka mitatu nyuma kiwanda kimoja cha samaki peke yake kilikuwa na uwezo wa kukata tani 250 kwa siku kikiwa kimeajiri wafanyakazi wasiopungua 600; na hawa walikuwa ni vijana kabisa wa kike na wa kiume. Leo tunapozungumza hapa, kiwanda kimoja cha samaki kati ya viwanda saba kinakata tani zisizopungua 20 mpaka 72 kwa siku, kikiwa kimepunguza wafanyakazi kutoka 500 mpaka 750 kufikia wafanyakazi 96 mpaka120. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba vijana wengi wamepoteza ajira lakini vijana wengi hawana pa kwenda ndiyo sababu unaona Mji wa Mwanza unazidi kujaa kwa vijana ambao hawana kazi, kila mmoja anatamani kufanya biashara ya umachinga, kila mmoja anatamani kufanya biashara ya umama lishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu! Tatizo liko kubwa! Mheshimiwa Waziri viwanda hivi vinakufa kwa sababu zao la samaki linapungua. Zao la samaki linapungua kwa sababu gani? Uvuaji wa njia za sumu umekuwa ni mkubwa zaidi na badala yake samaki hazipatikani kwa njia rahisi, lakini wenzetu wamezalisha samaki hizi na kwenda kuzivuna na kuzipanda makwao, leo unaweza kupata samaki wengi sana kutoka Ugiriki na kutoka Urusi na wameongeza ushindani zaidi kwenye soko letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, quality ya samaki wanaovuliwa sasa kwa sababu uvuvi haramu umekithiri, hii sumu inasambaa sana. Unapozungumzia uvuaji katika Ziwa Victoria, mikoa hii inayotumia sana uvuaji huu kwa Ziwa Victoria, lakini zipo nchi za jirani, Uganda na Kenya, wanafanya biashara kama sisi. Sasa wazo langu hapo Mheshimiwa Waziri, ni lazima tuangalie njia mbadala. Tutafanyaje kuhakikisha tunaokoa, uvuvi huu haramu unaondoka na tunabaki na uvuvi sahihi ambao unaweza kusaidia viwanda hivi?
Mheshimiwa Waziri, Mwanza kwa sasa ukipata mbinu mbadala ya kuhakikisha viwanda hivi vinaendelea na uzalishaji wake kama zamani, vinarudisha ajira kubwa iliyoangaka. Huna sababu ya kufikiria kujenga viwanda vipya vya samaki kwa sasa Mwanza. Hivi tulivyonavyo, kama tunakwenda kujenga viwanda vipya, hivi tunaviweka kwenye kundi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kiwanda cha Mwatex pale, miaka kumi iliyopita, tangu tukibinafsishe mpaka leo, wafanyakazi kutoka 700 na kitu mpaka 30 na kitu kwa siku. Hata walioondoka hawajalipwa mpaka leo, imekuwa ni kero na kasheshe kila kukicha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tuangalie hivi tulivyonavyo kwanza kabla ya kufikiria mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunacho kiwanda cha Tanneries pale, nilikuwa nataka kumpa taarifa rafiki yangu Mheshimiwa Msigwa, bahati mbaya tu nilichelewa, nilitaka tu nimtaarifu kwamba unapozungumza Kiwanda cha Tanneries hakihusiki na kuzalisha nyama, bali kinahusika na kutengeneza na kuzalisha mazao yanayotokana na ngozi. Kiwanda hiki kimeuzwa na kimekuwa godown, hakuna shughuli inayofanyika pale na tumepoteza vijana wengi ambao naamini Serikali mngefikiria vizuri, leo vijana wetu wangekuwa wanafanya kazi pale. Kwa maana siyo kwamba ng‟ombe nao wamekufa, ngozi hazipatikani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, majeshi yetu leo yangekuwa yanapata bidhaa za viatu kutoka pale, mikanda yao wangetoa pale na kadhalika. Sasa hivi tunavyozungumza, makampuni ya ulinzi yamekuwa mengi na maarufu sana nchini hapa. Wote hawa wanahitaji bidhaa za viatu hizi na mikanda yao ni hii hii ya bei za kawaida. Leo hata mikanda tunaagiza kutoka China na bahati mbaya sana inakuja ya plastiki ambayo haidumu, unanunua leo, kesho imekatika inabidi ununue mwingine.
Mheshimiwa Waziri nakuomba, tunayo kila sababu ya kuangalia umuhimu wa kiwanda hiki ambacho kilikuwa kinasaidia watu wa Mwanza kupata ajira na kadhalika, uangalie uwezekano wa kukifanya kirudi na sisi tukitumie kwa manufaa ya Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza suala la uboreshaji wa viwanda tulivyonavyo, tunazungumza suala la anguko kubwa la ajira. Kama ajira hii ambayo vijana wengi wanaitegemea, leo kila tukija hapa, nami kila nikisimama nazungumza juu ya ukuaji wa Mji wa Mwanza. Leo yapo maeneo tupetenga kwa ajili ya EPZ, hizi EPZ zinafanya nini? Tunajenga leo, tunatenga leo, matokeo yake ni baada ya miaka 30. Waachiwe watu maeneo haya wafanye biashara zao nyingine za kawaida, maana kuendelea kutunza maeneo makubwa, na mimi nikupe mfano, walikuja watu wa NDC toka mwaka 1974 wakachukua eneo la zaidi ya ekari 305, sawa na ekari 705. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo haya yamekaa toka miaka ya 1980 mpaka leo, eneo halijaendelezwa na tumeambiwa eneo hili ni kwa ajili ya viwanda vidogo vidogo. Pia maeneo mengi yanayochukuliwa hayalipwi fidia kwa wakati. Tunajua Halmashauri zetu hazina uwezo mkubwa wa ukusanyaji wa mapato. Hebu nikuombe Wizara yako ione umuhimu na maana halisi ya kuhakikisha maeneo yote yanapotengwa kwa ajili ya viwanda, aidha vidogo vidogo au viwanda vikubwa, tafsiri yake tunataka kupunguza mzigo, lakini tunataka kukuza uchumi, zaidi ya yote tunataka kuajiri vijana wengi zaidi ili tufikie kwenye malengo ambayo ilani yetu inasema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatuwezi kuboresha maeneo haya, hatuwezi kuokoa kundi kubwa la vijana ambao wanamaliza vyuo. Sio wanaomaliza vyuo tu, wako watu wana vipaji wanaweza kufanya kazi. Viwanda hivi tunavyovizungumza ni viwanda vinavyochukua watu wenye tabia tatu, wenye elimu ya chini, elimu ya kati na elimu ya juu, wote hawa wanataka ajira. Ni lazima tufike sehemu, kama tunataka kuepukana na matatizo ya msongamano wa vijana machinga, mama lishe na kadhalika kwenye maeneo mengi, lazima tuhakikishe tunajenga viwanda, lazima tuhakikishe viwanda hivi vinahimishwa, vinakuwa sawasawa na vinafanya kazi zake kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nakuomba tu kwamba nitakuunga sana mkono lakini kubwa ninalotaka kulisema, Mheshimiwa Mwijage sisi tuna imani na wewe. Tunayo imani kubwa, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano amekuamini na sisi tunakuamini. Imani yetu tuliyonayo kwako tunataka kuona, tunajua huu ndiyo mwanzo, tunataka kuona hapo ulipo na hayo unayoyasema unayasimamia, unayafanyia kazi. Na wewe ni jembe la shoka, hatuna shaka, hizi nyingine ni kelele tu tumeshazizoea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka uone watu hawana adabu, haiwezekani unazungumza, unatukana, unamaliza unaondoka bila kusubiri majibu. Hawana nia njema na Watanzania hawa.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Meshimiwa Mwenyekiti, tunataka watu ambao ukitoa hoja ya misingi kwa ajili ya Watanzania, ukitoa hoja kutetea vijana kwamba wanatafuta ajira, lazima ubaki upate majibu yake. Waangalie wako wapi? Mheshimiwa Kubenea yuko wapi hapa? Mheshimiwa Msigwa yuko wapi hapa? Wametukana, wameondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka niseme Waheshimiwa Wabunge, iko tofauti na lazima tukubali. Tofauti ya Mbunge wa CCM na Mbunge wa Upinzani ni kubwa na itabaki pale pale. Sisi ndio Wabunge wenye Serikali na hiyo ndiyo tofauti, hakuna namna nyingine. Sisi ndio wenye Serikali, ni lazima tuiunge mkono Serikali hii, tufikie malengo ya watu wetu kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mhesimiwa Mwenyekiti, mtu mwingine, rafiki yangu Mheshimiwa Mussa pale anashangaa kila tunachokisema tunazungumzia ilani. Kwenye ushindani kule si kila mtu alinadi ilani yake. Haya ndiyo matunda ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Leo ukisimama hapa unazungumza, mwisho wa siku unaomba. Ndugu yangu Mheshimiwa Mussa ameomba reli ya kati ianzie Tanga. Bila Ilani ya CCM usingeomba reli ya kati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwashukuru sana na niendelee kuhimiza, naunga mkono bajeti asilimia mia moja, viwanda kwa ajira za vijana wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia angalau kwenye Wizara hizi mbili niweze kusema maneno machache.
Kwanza nianze kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano, Mheshimiwa Rais pamoja na Baraza lake lote la Mawaziri kwa namna ya kipekee ambavyo wamekuwa wakifanya shughuli zao na kuwajibika kwa kiwango cha hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii kuwashukuru sana wapigakura wa Jimbo la Nyamagana kwa kazi kubwa sana waliyoifanya. Niwahakikishie kwamba ninapokuja Bungeni hapa, nakuwa nimekuja kazini na kazi moja kubwa ni kusimamia na kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kuwalipa yale waliyoyafanya baada ya tarehe 25 Oktoba, 2015. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa shughuli nyingi za kimaendeleo ambazo imeendelea kuzifanya katika Jimbo la Nyamagana, lakini yapo mambo machache ambayo tunapaswa kushauriana na kuambizana ili tuweze kuyarekebisha na tuweze kuendelea vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kidogo juu ya habari ya mapato, nizungumze juu ya habari ya ajira kwa vijana, lakini nizungumze juu ya namna ambavyo Halmashauri zinaweza kuongeza mapato kutokana na uwekezaji wa taasisi mbalimbali.
Sote tunafahamu, Jiji la Mwanza ni sehemu ya Mkoa wa Mwanza ambao ni mji wa pili kwa ukubwa Tanzania; lakini ni ukweli ule ule usiofichika kwamba Nyamagana na Jiji la Mwanza ndiyo mji unaokua kwa kasi zaidi Barani Afrika katika nchi yetu ya Tanzania. Tafsiri yake unaipata katika ongezeko la watu; 3% ya kuzaliana na 8.2% ya wahamiaji na wageni wanaoingia kila wakati kwenye Jiji la Mwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie nafasi hii kuikumbusha Serikali yangu, Jimbo la Nyamagana ni sehemu ambayo ni kitovu cha Mikoa ya Kanda ya Ziwa. Unapoanza kuzungumza habari ya msongamano wa watu, habari ya msongamano wa vifaa wa vyombo vya usafiri, lakini habari ya msongamano wa wafanyabiashara ndogo ndogo ambao kwa kweli huwezi kuwaondoa kwa sababu ndiyo sehemu wanayoweza kupata fursa nyingi zaidi katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii kuiomba Wizara ya TAMISEMI kwamba Halmashauri peke yake haiwezi kukabiliana na taizo hili, lakini kupitia masuala mbalimbali, kwa mfano, tunapozungumza juu ya uboreshaji wa Miji na upanuaji wa Mji, naiomba Wizara ya TAMISEMI kupitia kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene; mara kadhaa tumekuwa tunazungumza na unanipa ushirikiano wa kutosha, nakupongeza sana. Sina shaka Halmashauri hizi zimepata dawa ambayo kwa kweli ukiendelea hivi, naamini tutafikia kwenye lengo tunalolitazamia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko tatizo kubwa sana la wafanyabiashara ndogo ndogo na leo nitajikita hapa sana. Bila kutafuta ufumbuzi kutoka juu, bila kuisaidia Halmashauri kuweza kupanua Mji; tunapozungumza kupanua barabara ya kutokea Buhongwa kupita Kata ya Sahwa kwenda Lwanima, kutokea Igoma kuunganisha Fumagila kukamata barabara inayotoka Usagara kwenda Kisesa; tusipopanua Mji hatuwezi kuwaondoa machinga katikati ya Mji! Tusipopanua Mji hatuwezi kupanua fursa za vijana ambao wanapaswa kujitanua na kufuata yaliko makazi! Huwezi kuwaondoa machinga kuwapeleka sehemu ambako hakuna wakazi, hakuna watu, hakuna biashara! Inakuwa ni vigumu sana; lakini ndio wakwetu hawa, wanaingia kwa kasi!
Mheshimiwa Mwenyekiti, unakumbuka miaka ya nyuma, ni miaka michache tu iliyopita, watu wengi walitumia nafasi hii kujinufaisha sana kupitia vijana hawa wanyonge na maskini wanaotafuta maisha yao ya kawaida. Kwa sababu waligundua ukweli na kuamini Chama cha Mapinduzi peke yake kupitia watu wake wanaweza kukisaidia, Nyamagana wameamua kufuta habari ya upinzani na wakakirudisha Chama cha Mapinduzi. Sasa ni lazima tuwatendee haki kwa kuwaboreshea miundombinu, kuimarisha maeneo yao ya biashara ili wafanye kazi zao vizuri na Mji ubaki unapumua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naomba nizungumze juu ya uwekezaji. Tunafahamu Halmashauri hizi hazina mapato mengi. Nawashukuru sana LAPF kwa uwekezaji wao mzuri na mkubwa, nafahamu wamefanya Morogoro na baadaye wamekuja kufanya Mwanza. Tumefanikiwa kujenga Shopping Mall ya kisasa, Eastern Central Africa unaikuta Mwanza peke yake. Hii itatusaidia kuongeza ajira zaidi ya vijana 270.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni nini? Kuwepo kwa mall hii peke yake siyo tu kuongeza ajira, inaongeza kipato kwenye Halmashauri kwa sababu Halmashauri imewekeza kupitia ardhi yake, LAPF wamewekeza fedha. Kwa hiyo, tunagawana mapato siku ya mwisho na Halmashauri zinaendelea ku-generate income tofauti na kutegemea ushuru mchache ambao unatokana na kero mara nyingi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la afya. Sote tunafahamu namna ya kumlinda mama na mtoto wakati wanapojifungua. Tunapozungumza kuboresha zahanati na vituo vya afya, tunapozungumzia habari ya maduka ya dawa, tumeanzia ngazi ya juu sana. Hatukatai, ni vizuri hatua zimeanza kuchukuliwa, lakini unapoboresha kwenye Hospitali ya Mkoa ukasahau kuboresha kwenye Hospitali ya Wilaya, tafsiri yake ni kwamba mzigo wote wa Wilayani unaupeleka Mkoani; unaondoa chini huku ambako watu wengi wanahitaji msaada, hatuwezi kufanikiwa. Hii ndiyo maana tunasema, siyo rahisi sana, lakini tunajitahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niwashukuru sana kwa kuanza kupeleka maelekezo kwa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa. Hawa wakiwajibika na wao sawasawa Halmashauri zitapunguza mzigo kwa sababu watakuwa wanashirikiana katika kuhakikisha wanapeleka maendeleo kwa wananchi na mifano mizuri mnayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu, kwenye Jimbo la Ilemela pale kwa mama yangu, Mama Angelina Mabula, iko zahanati moja ya muda mrefu, Zahanati ya Sangabuye. Zahanati hii imeanza kitambo, lakini mpaka leo inapata fedha za zahanati wakati ni kituo cha afya. Halikadhalika zahanati iliyoko kule Nyamuhungolo, hakuna wataalam lakini inavyo vifaa vyote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie tu kwa kusema nikiwa naendelea na mimi nashangaa sana kwenye suala la elimu; tumesema elimu ni bure, watu wanalalamika. Wakati inaanzishwa, wakati tuko kwenye kampeni, watu walikuwa wanajinasibu kutoa elimu bure, leo wanashangaa Serikali ya CCM kutoa elimu bure, wanasema ni fedha za walipakodi. Unapozungumza elimu bure, tafsiri yake ni nini? Nani unataka atoe fedha mkononi kama siyo Serikali yenyewe? Na mimi nashangaa! Nilikuwa najiuliza, hawa watu ni kiumbe cha namna gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tukitaka kuangalia hapa; namshukuru sana Mheshimiwa Zitto Kabwe kwa kuona thamani na umuhimu wa elimu hii ambayo CCM imesema, elimu ya kuanzia chekechea, msingi na sekondari ni bure. Kwake kule kwenye Halmashauri akiwa na mwaka mmoja tu na Chama chake, amesisitiza kuanzia kidato cha tano na cha sita. Ninyi mna miaka 23 mmefanya nini kwenye elimu kama siyo kulalamika leo? Nimekuwa najiuliza, tunahangaika hapa, kila siku ni kutukana, kulalamika! Tunataka kujua! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ungetusaidia. Mara zote mimi nimejiuliza, hawa UKAWA ni viumbe wa namna gani? Ni chura au ni popo hawa? Maana ndiyo peke yake huwezi kujua! Chura anabadilika kila wakati, lakini kinyonga huwezi kujua! Kinyonga anabadilika kila wakati, lakini popo huwezi kujua kama ni ndege au ni mnyama? Kwa hiyo, hii tunaipata wazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 22 Aprili, 2016 hapa Mwenyekiti wao alisema, katika mazingira kama haya, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni haiko tayari kuendelea kushiriki na uvunjaji wa Katiba, Sheria na haki za msingi za wananchi. Leo wanashiriki hapa, wameungana na sisi, hawajaungana na sisi? Ukishindwa kupambana naye, ungana naye. Hii ndiyo dhana halisi! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hawa wameshashindwa kupambana na sisi…
Nawashukuru kuendelea kuungana na sisi! Na mimi nakushukuru sana. Dhamira ya Chama hiki ni kuendelea kuongoza na kuweka maendeleo sawasawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa namalizia, namshukuru sana Waziri wa Wizara ya Michezo, Habari, Sanaa na Utamaduni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Nyamagana tumehangaika kwa muda mrefu juu ya uwanja wetu wa Nyamagana, leo ninavyozungumza tayari nyasi ziko bandarini na muda mfupi kazi inaendelea katika uwanja wa michezo wa Nyamagana. Tafsiri yake, tunataka kuimarisha! Ukiimarisha michezo umekuza ajira kwa vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuokoa muda nianze tu kwa kutoa pole kwa Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Mkurugenzi pamoja na Madiwani, lakini kwa wananchi wa Kata ya Mandu kwa kuondokewa na Diwani wao mpendwa Mheshimiwa Wambura, naamini Mungu ataendelea kuwatunza vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nashukuru na mimi kwa kupata fursa ya kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI. Pamoja na mambo mengi iliyonayo, lakini ningejielekeza kwenye mambo machache. La kwaza, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii ya TAMISEMI kwa namna ya kipekee ambavyo wamekuwa
wakijishughulisha katika kuhakikisha wanatatua changamoto tulizonazo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo moja kubwa ambalo naanza nalo ni juu ya usafi wa mazingira. Nami nimeshangaa kidogo, kwenye kitabu cha taarifa, Mheshimiwa Waziri kama usipojitengenezea mazingira ya sisi kukusemea na mwenyewe huwezi kujisemea, Serikali hii kwa mwaka huu wa fedha tulionao kwenye Majiji manne na Manispaa tatu, imetumia fedha nyingi sana katika kuhakikisha inaboresha taratibu za upatikanaji na uzoaji wa taka na kuboresha miji na majiji.
Mheshimiwa Spika, nimeangalia taarifa hii imezungumza mistari michache sana, inataja tu kununua vifaa. Vifaa vilivyoko Mwanza peke yake ni vya zaidi ya thamani ya shilingi bilioni nne. Kuna truck zaidi ya 12, kuna excavator, duzor, compactor na kadha wa kadha na sasa tunajenga dampo la kisasa kuhakikisha usafi wa Mji. Haya yote nilitegemea niyaone na haya yamefanyika Arusha, Tanga, Mbeya, Dodoma, Mtwara pamoja na Kigoma. Sasa usipojisifia wewe Mheshimiwa Waziri, sisi tutakusifia mpaka lini?
Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze kwenye suala la wafanyabiashara ambayo inaitwa sekta isiyo rasmi ya wafanyabiashara ndogo ndogo Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika, wafanyabiashara ndogo ndogo kwa sasa ingewezekana wakatambuliwa kama Sekta Rasmi, kwa
sababu wako zaidi ya 30,000 nchini kote. Mara kadhaa tumekuwa tunawachukulia kama watu ambao hatuoni umuhimu na thamani yao na ndiyo maana mara kadhaa wamekuwa wakifukuzwa na mgambo, wamekuwa wakipigwa mabomu, lakini mwisho wa siku wanaharibiwa
mali zao, kunyang’anywa na kuteketezwa. Siyo wao tu, hapa namwongelea Mmachinga wa kawaida, mama lishe, baba lishe na kadhaa wa kadhaa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa sote tunafahamu kwa sasa suala zima la Halmashauri zetu katika kukusanya kodi, limekwenda chini sana na mfano mzuri, ukichukua tu takwimu za Mkoa wa Mwanza na Halmashauri zake zote kwa ujumla, mwaka 2016/2017 tulitazamia kukusanya shilingi
bilioni 34, mpaka leo tunazungumza, taarifa inasema tumekusanya shilingi bilioni 16. Tunakusudia bajeti ya mwaka 2017/2018 tukusanye shilingi bilioni 35, ongezeko la milioni 600 peke yake.
Mheshimiwa Spika, nataka kusema nini? Machinga hawa wa leo ambao tunawaona sio watu muhimu kwenye shughuli zetu, tunaweza tukawafanya wakawa sehemu kubwa sana ya kipato kwenye Halmashauri ambazo Machinga hawa wamekaa mjini sana.
Mheshimiwa Spika, ukichukulia Mwanza peke yake, nimeangalia Dar es Salaam, Mbeya, Arusha na maeneo mengine ikiwemo na Dodoma. Kwa Mwanza peke yake, chukulia tunao Machinga 5,000. Machinga biashara yao inajulikana ni kwa siku, tu-assume Machinga mmoja kwa siku popote alipopanga alipie shilingi 1,000 peke yake ya kile kieneo kidogo ambacho amekitenga.
Mheshimiwa Spika, kwa Machinga 5,000 tutakusanya shilingi milioni tano, mara 26 kwa mwezi ukiondoa Jumapili, unatengeneza zaidi ya shilingi milioni 130; kwa mwaka mzima Halmashauri ya Jiji la Mwanza inaweza kuingiza zaidi ya shilingi 1,200,000,000. Fedha hizi hatutakaa tutegemee fedha za Serikali kuwasaidia wafanyabiashara ndogo ndogo, lakini kuwasaidia kuweka miundombinu ambayo kesho tutawapeleka wakakae katika miundombinu iliyo bora na sahihi (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kupitia mfumo huu, tukikubali haya maeneo tuliyowapa sasa kwa muda wakakaa kwa miaka mitatu mpaka miaka mitano; tunaweza kutumia fedha zao wenyewe kujenga miundombinu rafiki na wao wakawa tayari kwenda kufanya biashara kwenye maeneo yale. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba hili linasambaa maeneo yote ya nchi ambayo mara nyingi ni maeneo ya Miji. Tunaweza kufanya hivi na tukawasaidia wafanyabiashara hawa. Kwanza watakuwa na uhakika na maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kufanyia biashara. Wakiwa na uhakika, wamekuwa na uhakika na shughuli yao na kesho yao kwa sababu tunataka tuwasaidie.
Hili linajidhihirisha! Ukiangalia fedha za vijana na wanawake, kati ya shilingi 56,800,000,000; tumepeleka shilingi bilioni 27.5 peke yake, sawa na asilimia zisizozidi 27.
Mheshimiwa Spika, sasa kwa kufanya hivi pia tutakuwa tumemsaidia sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mavunde pale anayehangaika na kutatua kero za vijana kila siku. Kwa sababu siyo kweli kwamba ipo siku Halmashauri zitafikia asilimia mia kupeleka fedha za wanawake na vijana
kwa sababu mahitaji ni mengi kuliko kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimeongea sana hapa kwa sababu ni changamoto kubwa sana na sisi tunawaogopa kwa sababu hawa ndiyo watu ambao tunaamini wakitengenezwa vizuri, kwa haya tunayoyasema, Dar es Salaam kule Ilala peke yake, pale Kariakoo wanasema wana
Machinga zaidi ya 5,000. Ukiwafanyia utaratibu huu tunaouzungumza na wao watapata kipato, lakini na Manispaa nyingine pia pamoja na Majiji wanaweza kuwa na hatua kubwa sana ambayo itawapelekea kupiga hatua kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nigusie kidogo juu ya suala la ufya. Uboreshaji wa sekta ya afya, kwenye ripoti inaeleza wazi kwamba imejikita na inaelekeza katika kujenga vituo vya afya zaidi ya 244 lakini kujenga hospitali zetu za rufaa. Sasa ni lazima tukubali, tunapojenga Hospitali za Rufaa ni lazima pia tuwe tayari kuimarisha.
Mheshimiwa Spika, mwaka uliopita tulisema tutajenga zahanati na kituo cha afya kwenye kila Kata. Sasa mpaka leo tunatazamia kujenga Vituo vya Afya 244. Tunavijenga kwenye Kata zipi? Waziri atakapokuja tunaomba pia tujue ni Majiji gani na Halmashauri zipi, Kata zipi zitakazofaidika na hospitali hizi 244. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia Hospitali za Wilaya; tunazo Hospitali za Rufaa za Kanda na Mikoa. Leo kama hatuna Hospitali za Wilaya kwenye Wilaya zetu, ni vigumu sana kutoa huduma zilizo bora kule kwenye hospitali zetu za rufaa.
Mheshimiwa Spika, ukienda pale Wilaya ya Ilemela, ni Wilaya mpya, haina Hospitali ya Wilaya, wanategemea Hospitali ya Jeshi. Tunafahamu Jeshi namna na wao walivyo na shughuli zao nyingi, tuna wajibu wa kuhakikisha Wilaya ya Ilemela inapata Hospitali ya Wilaya ambayo kimsingi imeshaanza kujengwa kwenye eneo la Busweru. Siyo hivyo tu, wamejikakamua kwa namna wanavyoweza, wameanza na jengo la wagonjwa kutoka nje, lakini uwezo wa kukamilisha kwa gharama ya shilingi bilioni tatu haiwezekani.
Mheshimiwa Spika, tunaomba fedha hizi zinazokwenda kujenga Hospitali za Rufaa, tuelekeze pia kwenye Hospitali za Wilaya ili tupunguze mzigo hata kwenye hizi hospitali za rufaa tunazozijenga kuanzia huku wilayani.
Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo, leo kwenye Jimbo la Nyamagana kupitia Mfuko wa Jimbo na wadau mbalimbali tunayo maboma manne kwa ajili ya vituo vya afya; Kata ya Buhongwa, Kata ya Lwang’ima, Kata ya Kishiri na Kata ya Igoma, tunataka kukamilisha, tunayamaliza vipi?
Uwezo wa Halmashauri zetu kukusanya mapato kwa nguvu unaelekea kuwa siyo mzuri sana. Ni lazima tuhakikishe tunajikita kwenye kuboresha hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunazungumza sasa hivi, tunaelekea kwenye kukusanya kodi kwa wafanyabiashara ndogo ndogo waanze kulipa service levy, wenye leseni za kuanzia shilingi 40,000. Mfanyabiashara mwenye saluni yenye kiti kimoja au viti viwili anayelipa leseni ya shilingi
40,000; baada ya miezi mitatu anatakiwa alipe service levy.Ni wafanyabiashara wa namna gani tunaowakusudia?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashauri…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niunge hoja mkono na ninashauri hayo yafanyiwe kazi. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie walau maneno machache katika hii Wizara muhimu kabisa juu ya masuala mazima ya miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa maneno machache ya shukrani nikimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara husika juu ya kazi njema na nzuri wanazoendelea kuzifanya katika kuhakikisha suala zima la miundombinu ya barabara, usafiri wa maji na nchi kavu unafanyiwa kazi na unakamilika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na shukrani hizi nafahamu uko upanuzi wa uwanja wa ndege, tumeziona fedha pale Mwanza na niwapongeze sana kwa kutumia zaidi ya shilingi bilioni 18 kwa fedha za ndani na shilingi bilioni tano peke yake fedha za nje. Hii tafsiri yake ni kwamba zoezi hili linaweza kukamilika kwa wakati kama tulivyokusudia tofauti na tungetazamia sana kutumia fedha za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili niwashukuru kwa upanuzi wa barabaraya kutoka Furahisha kwenda Kiwanja cha Ndege, kwa barabara nne. Ni kitendo kizuri ambacho kitaendelea kuujenga Mji wa Mwanza uendelee kubaki kuwa mji bora na mji wa pili kwa ukubwa Tanzania katika kuhakikisha shughuli zote za maendeleo na uzalishaji mali za kiuchumi zinazoifanya Mwanza kuwa mji wa pili katika kuchangia pato la taifa iendelee kuongeza zaidi ya pale ilipo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kufikia malengo haya tunayoyafikiria liko suala la barabara za kupunguza msongamano. Mara kadhaa nimekuwa nikisema, lakini nasikitika sana kwa sababu hata vikao vya RCC Mwanza mara kadhaa vimeshafanya mapendekezo zaidi ya vikao miaka mitatu mfululizo. Vinafikiri kupandisha barabara ya kutoka Buhongwa kupita Lwanima, Sawa, Kanindo kutokea Kishiri – Igoma na Fumagira kama itajengwa kwa kiwango cha lami, barabara yenye urefu wa zaidi ya kilometa 11.8 inaweza kusaidia sana Mji wa Mwanza kufunguka na tukaendelea zaidi kuwa kwenye hali nzuri ya kiusafiri. Lakini hii ni pamoja na barabara kutoka Mkuyuni kupita Igelegele - Tambukareli - Mahina na kwenda kutokea Buzuruga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiofichika kwamba mji wa Mwanza unakua, na kama mji wa Mwanza unakua na tunatambua ndiyo mji ambao uko kwenye kasi ya kuchangia pato la Taifa, sioni tunapata kigugumizi gani kuhakikisha kwamba barabara hizi zinafunguka kwa urahisi ili unapokuza uchumi wa Mwanza unaendelea kuchangia/ kuongeza pato la Taifa kutokea kwenye Mkoa huu ambao ni Mkoa wa pili kwenye kuchangia pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimesema hapa ni ukweli usiofichika kwamba Mwanza ndiyo Mji pekee unaokua kwa kasi zaidi katika East Africa. Ukichukua Afrika ni mji wa tano katika Majiji kumi yanayokuwa kwa kasi. Leo hatuangalii kama kuna umuhimu wa kuendelea kuitengeneza Mwanza iendelee kuwa mji wa tofauti na mji ambao utakuwa unaendelea kutoa matunda bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapoongelea kukua kwa mji unaongezea pia kuongezeka kwa watu. Sasa hivi tunazo barabara mbili peke yake, iko barabara ya Kenyatta na barabara ya Nyerere, hizi ndizo barabara peke yake unazoweza kujivunia leo Mwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee tu kusema, naamini Mheshimiwa Waziri analitambua hili na tusifikiri hata siku moja kwa fedha za Mfuko wa Barabara hizi zinazokuja kwenye Majimbo na Halmashauri zetu, shilingi bilioni mbili au tatu zinaweza zikasaidia kupunguza msongamano. Fedha hizi ni kidogo, kama zinaweza kufanikiwa sana zitatusaidia tu kutengeneza barabara za kilometa 0.5, 0.2 au 0.3 na kadhalika, hatutaweza kufikia malengo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo barabara ya kutoka Mwanza Mjini, naizungumzia barabara ya Kenyatta, kuja kutokea Usagara ambako unakwenda kupakana na Misungwi barabara hii ni finyu sana, lakini yako maeneo upanuzi wake unahitaji gharama kubwa sana. Kwa hiyo, kama hatuwezi kuitengeneza kwa maeneo kadhaa na yenyewe ikawa kwa njia nne hatutakuwa tumesaidia sana. Kwa hiyo, niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri, wakati wanakamilisha ujenzi wa njia nne kutoka Furahisha kwenda Airport tuifikirie kwa namna nyingine barabara ya Kenyatta, nazungumzia kutoka mjini kati kwenda Mkuyuni - Butimba, Nyegezi - Mkolani - Buhongwa na hatimaye kukutana na Misungwi ili tuweze kuwa kwenye mazingira ambayo yanafanana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze habari ya bandari. Imesemwa hapa, katika bandari hizi zinazojengwa, Bandari za Mwanza zimesahakuwa ni za kizamani sana. Lakini tukiboresha Bandari hizi za Mwanza, naongelea South Port na Mwanza Port, tutakuwa tumesaidia kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunafahamu mizigo mingi inayotoka Kenya, Uganda wamekuwa wakitumia bandari hizi, lakini hata kukamilika kwa reli ya kutoka Dar es Salaam itakapokuwa imekamilika vizuri bandari hizi bado ni chanzo kikubwa sana. Juzi tumemsikia Mheshimiwa Rais wakati anazungumza na Rais wa Uganda, amezungumzia juu ya bandari ya nchi kavu iliyoko kwenye Kata ya Lwanima.

Mimi nioneshe masikitiko yangu makubwa sana kwa Mheshimiwa Waziri, bandari hii ambayo tayari miaka minne iliyopita toka mwaka 2012/2013 mpaka leo 2017 wananchi kutoka kwenye mitaa minne, nazungumzia wananchi wa Kata ya Lwanima kutoka kwenye mitaa ya Ihushi, Isebanda na Nyabahegi wameshafanyiwa uthamini miaka minne leo lakini bado hawajalipwa hata shilingi moja, Wameendelea kulalamika juu ya bandari ya nchi kavu na mbaya zaidi, hivi ninavyozungumza ziko taarifa kwamba ujenzi wa bandari hii unataka kuhamia Misungwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Naomba nimpe taarifa kabisa hapa Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Kata ya Lwanima mitaa ya Isebanda, nyabahushi hawatakubali kuona mradi huu unahama unakwenda kwenye kata na wilaya nyingine kwa sababu wamekuwa wavumilivu. Wamesubiri kwa muda wa miaka minne wakiwa na matumaini na Serikali yao kwamba watalipwa fidia na ukamilikaji wa bandari hii ya nchi kavu utaongeza ajira, shughuli za uzalishaji kwenye maeneo yao na tutapata fedha kwa ajili ya wananchi wetu, lakini tutakuwa tumeendelea kuchangia pato kwa Serikali yetu na kuhakikisha mazingira haya yanaboreka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii lazima tukubali, ndiyo maana nasema mji wa Mwanza leo itakuwa ni ajabu sana, ukitaka kuangalia tuna kilometa ngapi za lami. Mji unaoitwa wa pili kwa ukubwa haufikishi kilometa 50 za barabara ya lami, hii ni aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia barabara za kupunguza msongamano zinarundikwa sehemu moja tu zaidi ya kilomita mia na kitu. Hivi leo mkitupa Mwanza hata kilometa 20 peke yake kupunguza misongamano sisi hatutafurahi? Wananchi hawataona thamani kubwa ambayo na wao wanashughulika katika kuhakikisha nchi yao inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo haya mambo ni lazima tukubaliane; kasungura tunafahamu ni kadogo, tuko kwenye jitihada za kukusanya mapato lakini hao hao wanaochangia mapato lazima tuwape nafasi na wao wafaidi haka kasungura kadogo hata kwenye kukagawana ukucha, kapaja na kadha wa kadha ili waweze kufikia malengo ambayo wanayakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la fidia naomba litazamwe kwa kipekee sana. Nimelisema kwa haraka kwasababu ya muda lakini haikubaliki wala haiwezi kueleweka miaka minne watu wamekaa wanasubiri fidia halafu wasifikie mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho, mara kadhaa tunaamini vikao vya RCC ndiyo vikao vikubwa na vinapokuwa vinatoa mapendekezo ni lazima yafikiriwe. Haiwezekani miaka minne mnatoa mapendekezo mbali ya barabara za kupunguza msongamano, kutoka Kenyatta kuendelea kwenye maeneo niliyoyataja lakini tulishawahi kupendekeza na hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, pale kwenye Jimbo la Ilemela kwa Mheshimiwa Angelina kiko kivuko kwenye Kisiwa cha Bezi ambako kuna wakazi zaidi ya 600 wamekuwa wanatumia mitumbwi ya kawaida. Hii peke yake inaonesha hali ya hewa wakati mwingine kwenye ziwa si rafiki, kuna kila sababu na kuna kila dalili kila wakati wananchi wanaendelea kupoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo baadaye walijadili kuhamisha kivuko kutoka Ukerewe ikaonekana haitakuwa sawa kwa sababu viko vingi na kadha wa kadha, lakini tumeahidiwa kupewa kivuko kipya. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aangalie kwa kipekee hiki Kisiwa cha Bezi kiweze kupata kivuko kipya ambacho kitasaidia kuokoa maisha ya Watanzania zaidi ya 600 wanaoishi maeneo yale ili waweze na wao kuishi kama wananchi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nilisema nizungumze machache haya kwa sababu naamini sote tunafahamu Mji wa Mwanza ulivyo, na asilimia kubwa hapa kila mmoja anatamani kupita Mwanza. Ni mji mzuri, tukiutengeneza vizuri utakuwa umekaa kwenye mazingira mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mungu akubariki sana, nakushukuru na naunga mkono hoja asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi jioni hii. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunipa afya, kwa sababu ya muda naomba nami kwa uchache sana nichangie Wizara hii muhimu kabisa, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya, katika kuhakikisha Tanzania ambayo tunatamani kuona imepangwa basi angalau wameanza na miji kadhaa ambayo kwa kweli kama tutafanikisha, tunaweza tukafikia hatua nzuri sana, kwa sababu tunafahamu upangaji wa ardhi unaendana na uimarishaji wa uchumi bora kwa maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli uisiofichika kwamba ardhi kubwa ya Tanzania bado haijapangwa sawa sawa na miji mingi tuliyonayo karibu miji yote hata Mji wa Dodoma ambao ulikuwa umeshaanza kupangwa kwa namna fulani, sasa hivi tunakoelekea kama hakutakuwa na usimamizi mzuri, tutegemee Miji aina ya Manzese na hapa Dodoma itakuwepo mingi sana na maeneo mengine mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa MWenyekiti, nianze tu tena nirudie kumshukuru Mheshimiwa Waziri, nakumbuka mwaka 2014, moja ya Miji ambayo ilikuwa imetengewa mkakati wa kupanga Mipango Miji Kabambe, Mji wa Mwanza ulikuwa ni moja kati ya miji karibu 14. Fedha nyingi sana ya Serikali imetumika pale katika kuweka mkataba na kampuni moja SULBANA International wa zaidi ya dola milioni tano za Kimarekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa sababu kwa mwaka huu peke yake, ndiyo mwaka ambao kazi kubwa sana imefanyika. Hivi tunavyozungumza karibu asilimia 90 ya kazi hii na timu hii kwa kweli ndugu Waziri naomba niipongeze sana timu aliyoikabidhi kazi hii kwa sababu inafanya kazi nzuri sana. Matarajio yangu ni kwamba kazi hii itakapokuwa imekamilika kwa sababu Mwanza ndiyo inaonekana kuwa ya kwanza, kwa namna Watendaji na Watumishi hawa walivyojitoa kufanya kazi hii usiku na mchana itakuwa imetuzalishia matunda makubwa zaidi na itapunguza kero nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko shida moja tu Mheshimiwa Waziri lazima tukubaliane kwamba mipango hii kabambe ya uboreshaji wa miji, pamoja na jitihada nyingi hizi ambazo inafanya kama tutaiacha, kama baada ya kukamilika hatutaona umuhimu wa kuipeleka kwa haraka ili ikamilike, tunakusudia miaka 20 itakuwa imetosha kabisa kuhakikisha kazi hii imekamilika na projection zake ziko wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema miaka 20 sasa hivi kwa Mwanza na Ilemela kwa maana ya Nyamagana na Ilemela ukitafuta makazi yako zaidi ya laki moja na sitini lakini wataalam wanatuambia miaka 20 ijayo tutakuwa na makaazi zaidi ya 520 wakati nyumba moja peke yake kuna wakaazi wasiopungua watano. Kadri miaka inavyokwenda watakuwa wanashuka kwa sababu tunaamini uchumi utakuwa umekua, elimu itakuwa imekua kubwa sana na kuzaliana kutapungua sana tofauti na sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, wito wangu kwenu ili hili liweze kufanikiwa vizuri ni lazima tuhakikishe, katika miji yote huu ndiyo mji wenye square metres za mraba 472 peke yake unaotakiwa kwenda kufanyiwa kazi, siamini kama unaweza kutuchukulia muda mrefu sana kuutengeneza Mji wa Mwanza ukawa ni moja kati ya Miji bora kabisa Tanzania kuliko ilivyo sasa. Tunaita Mji wa pili kwa ukubwa lakini ni kwa maandishi tu kutokana na uchangiaji wa uchumi siyo kwa muonekano wa mji kiuhalisia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo sasa, tunafahamu kwamba kwa nini sasa hivi tunalazimisha na tunasisitiza sana urasimishaji wa makazi. Utakubaliana na mimi kwamba tunahimiza urasimishaji wa makazi kwa sababu muda mrefu tuliacha ujenzi holela ukatokeza sana. Urasimishaji wa makazi tafsiri yake, tunataka tutoke kwenye makazi holela tuje sasa kuyafanya makazi haya yawe rasmi. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi, pamoja na jitihada zote hizi tunazofanya, namshukuru sana siku chache zilizopita amefanya ziara Mwanza, pale ametema cheche kali sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza na Mheshimiwa Waziri tayari invoice 19,000 zimeshaandaliwa na zaidi ya 3,000 zimeshakwenda kwa wananchi na 800 wameshalipa. Inaonekana kulikuwa na uzembe mkubwa. Kwa hiyo, tuendelee kutoa nafasi, lakini tuendelee kurudisha fedha hizi ambazo zinatokana na malipo ya ardhi, zitasaidia sana kuhakikisha kazi hizi zinakwenda haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tunataka kuimarisha makazi yetu vizuri tunaondoa makazi holela, liko tatizo moja kubwa na tatizo hili ndilo linaloikabili nchi nzima. Katika maeneo ipo michoro ilishaandaliwa miaka 10, 20 au 30 iliyopita lakini hayajawahi kuelekezwa sawasawa na mwananchi hajawahi kupata elimu vizuri kwamba hii michoro ikishapita huruhusiwi kujenga chochote humu ndani. Matokeo yake maeneo yamevamiwa na leo ukitaka kwenda kumwondoa mwananchi ambaye ulimfanyia mchoro miaka 20 iliyopita na hukumpa utaratibu unakwenda kuonekana ni mvamizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na urasimishaji makazi haya tunaulizana, ninayo maeneo kwenye Jiji la Mwanza na Jimbo la Nyamagana, ukichukua maeneo ya Mtaa wa Ibanda, Mtaa wa Swila, Mtaa wa Bukaga, Mtaa wa Kasese kwenye Kata za Nyegezi, Kata ya Igoma na Kata ya Mkolani, yako zaidi ya makazi elfu mbili, wapo wananchi wengi, walishajenga siku nyingi, michoro imetengenezwa. Hakuna namna tunaweza kuwasaidia wananchi hawa pamoja na kutaka kupanga Mji wa Mwanza vizuri kama hatutafumbua tatizo hili kubwa. Kinachoonekana leo ili tuweze kufumbua tatizo hili ni kwenda kuvunja makazi ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatutaendana na kasi ya Mheshimiwa Rais anayoizungumza, hatutaendana na kauli ya Mheshimiwa Rais ya kuwasaidia wanyonge. Sasa ni lazima tumsaidie Mheshimiwa Rais, ni lazima tuoneshe njia watalaam huku wanasema, kwa mfano miaka karibu 25 iliyopita eneo la Mkolani, Mtaa wa Kasese kuanzia kona ya Nyegezi pale Nyegezi, unakuja Butimba, unakuja Mkolani watu walishapima miaka mingi, Halmashauri wanasema mchoro wao unaonesha barabara ni mita 100, TANROADS wanasema barabara yetu ni mita 60. Nani anaingia katikati hapa kutatua mgogoro huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu kwenye mita zaidi ya 40, Halmashauri inasema hii ni buffer zone na watu wana miaka dahari mle ndani, leo wanatakiwa wavunjiwe nyumba zao, zaidi ya watu 1,600. Mheshimiwa Waziri najua yeye ni mtu wa huruma na hata akienda kwenye eneo hili mwenyewe anaweza kushangaa na akashangaa watalaam tulionao, kwa nini hawawezi kuchukua maamuzi mpaka wakubwa wafike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nimeshazungumza na mama yangu, jirani yangu, dada yangu Mheshimiwa Angelina, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, amesema wataliangalia kwa makini na nimeshazungumza na Mheshimiwa Waziri vizuri na najua ameshanisaidia sana. Kwa hiyo, naendelea kuwaomba tunao wajibu wa kuwasaidia Watanzania. Mwanza tunayotaka kuitengeneza leo uwe mji wa mfano hatutaonesha kama ni mji wa mfano kama hatutatatua changamoto hizi, badala yake tutaendelea kujaza kero kwa wananchi na hii itakuwa siyo sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia tu nizungumze suala moja ambalo amelizungumza Ndugulile hapa asubuhi. Bado hakuna elimu hata kwa watalaam wetu kule chini, tunazungumza asilimia 30 ya fedha za kodi ya ardhi zinazokusanywa, leo ukitaka kuuliza, hata Watendaji hawajui kama zile fedha hazitakiwi kurudi tena lakini watendaji wenyewe wanajua bado tunadai fedha nyingi. Fedha hizi zikija zitasaidia kumaliza kero ya kupima ardhi kwenye maeneo mengi ambayo tumeshindwa kupima mpaka leo, hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri waliangalie. Kama ilishaamriwa hivyo na Bunge hili likapitisha sheria, uende waraka kule chini kwa Watendaji kwenye Halmashauri walifahamu hili, kwamba fedha hizi wanazolipa mpaka leo Halmashauri ya Jiji la Mwanza imeshakusanya kodi ya ardhi zaidi ya bilioni moja na milioni mia tisa thelathini na mbili, lakini tunategemea asilimia 30 ya fedha zile iweze kutusaidia kukamilisha shughuli nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata zoezi la urasimishaji makazi kuna wakati lilikwama kwa sababu vifaa vilikuwa hakuna. Mheshimiwa Waziri alivyoondoka hatujui fedha zilipatikana wapi, computer zikanunuliwa, kila kitu kikawekwa na kazi hii niliyomwambia zaidi ya wananchi 800 wameshafanyiwa malipo, ndiyo matokeo ya matumizi ya fedha. Lazima tukubali kutumia fedha ili tujenge miji yetu na plan hizi tulizonazo ziweze kufanikiwa. Hatuwezi kufanikiwa kama hatujaona umuhimu wa ardhi na matumizi ya ardhi haya ni lazima tuyafanye for public consumption, tukifanya ni ya kwetu binafsi hatuwezi kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Jiji la Mwanza na Jimbo la Nyamagana wanayo masikitiko makubwa, yako maeneo yao wamekuwemo kwa muda mrefu lakini leo wanaonekana wavamizi, kwa sababu tu hatukuchukua hatua mapema, hatukutoa elimu mapema. Tutoe elimu, tuwaoneshe wananchi wapi panastahili na wapi pasipostahili, tutafanikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya. Tuendelee kuijenga Tanzania na wananchi wanyonge wapate tiba. Ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nitumie nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili angalau niweze kusema kidogo juu ya Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa ili haya ambayo tunakwenda kuyachangia utakapokuja Mpango kamili tuweze kuona mabadiliko lakini tuweze kuona hiki tunachokizungumza kinakwenda kufanyika kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu tuko hapa ndani kwa sababu ya kuzungumza lakini kwa sababu ya kuleta hoja ambazo zitawasaidia Watanzania. Naomba nianze tofauti kidogo na kuanza kwangu nataka kuzungumza juu ya suala zima la uboreshaji wa miji, majiji lakini namna ambavyo tunaweza kushughulika na mambo ambayo yanaweza yakatusaidia sana kwenye sekta ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimefurahi moja ya kati ya mapendekezo yaliyoko kwenye Mpango huu katika sekta ya ardhi inatambua na wajibu wake mkubwa ni kupanga, kupima na kumilikisha lakini tukifanikiwa kupanga, kupima na kumilikisha sisi wenyewe tunasema itakuwa ni sehemu nyingine ya mfumo wa uboreshaji na upatikanaji wa mapato mengi zaidi. Kwa nini nasema haya? Natambua Serikali inao mpango thabiti wa kuhakikisha maeneo ya Miji, Majiji, Manispaa na Miji inapimwa kwa kiwango ambacho kinastahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa upo mpango ambao unaendelea, mpango wa upimaji shirikishi ambao unamfanya mwananchi achange mwenyewe ili kuweza kupimiwa kwa sababu tu ya msingi kwamba maeneo mengi sana Serikali inatambua hayajapimwa. Liko tatizo moja hapa ambalo nilitamani sana kuliona kwenye Mpango humu ndani linawekewa mkakati thabiti.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni kuhakikisha hii premier ambayo inatokana na ada zinazoongezeka katika kulipia hati inaondolewa ili mwananchi huyu aweze kupata nafuu anapokwenda sasa kuchukua hati yake kimsingi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa sote tunafahamu mpango huu ukifanyika vizuri miji yetu mingi ambayo kiukweli ziko squatters za kutosha ikapimwa ikapangika na watu wote hawa wenye squatters wakishamaliza kupimiwa hizi ni fedha zingine ambazo Serikali inaweza kuzipata na zikatusaidia sana kwenye mapato. Kwa sababu ni ukweli usiofichika sasa hivi ziko fedha nyingi sana zinapotea kwenye kodi ya majengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao wanasafiri na ndege ukipita kwenye Miji ya Dar es Salaam, Mwanza, Dodoma, Arusha na miji mingine yote mikubwa unaweza kuona ni namna gani nyumba zilivyo nyingi lakini 70% ya nyumba hizi unaweza kukuta miji haijapangwa, nyumba hazitambuliki na badala yake hazilipi kodi.

Mheshimiwa Spika, sasa zoezi hili likifanyika vizuri sina shaka mwananchi mwenyewe atakuwa na uhakika na kile ambacho anakifanya lakini atakuwa na uhakika na makazi yake, lakini kubwa zaidi muda ambao kwa sasa Serikali imetoa na ndiyo mpango, kwenye Mpango ije ituambie huu muda utakuwa unakwenda kwa ukomo wa muda gani ili kuweza kusaidia wananchi hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu sote tunafahamu hata Mpango tunaokwenda nao upatikanaji wa fedha wenyewe haukidhi mahitaji na muda uliowekwa na Serikali. Sasa kule tunakokwenda lazima tuseme kwenye Mpango tunatazamia tuwe na muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, yako maeneo ambayo yana milima, mimi natoka Mwanza, Jimbo la Nyamagana, watu wengi sana wamejenga kwenye milima na hawa hatuwezi kuwaondoa kwa namna yoyote ile lakini tukijitahidi tukawapimia, tukarasimisha maeneo yao waliyopo yana uwezo wa kutengenezwa vizuri na eneo hilo tukawa tumesaidia Serikali ikakusanya kodi wananchi wakaishi kwa amani na wakaendelea kushughulika na maisha yao ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, nilikuwa najaribu kupitia mpango huu sijaona popote, tulizungumza hapa juu ya urasimishaji wa biashara na wafanyabisahara ndogo- ndogo, tunawazungumzia machinga, mama lishe, baba lishe na wengine wauza mbogamboga na matunda. Sasa kwenye mpango huu tunaoupendekeza sasa hivi hatuoni umuhimu wa kuweka wafanyabiashara hawa watengenezewe mkakati endelevu kuliko hivi walivyo sasa tutawaacha tu, tumesema wapewe vitambulisho, halafu miaka mingine inakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima tuhakikishe kwenye Mpango huu tunaoutafakari tuwatambue watu hawa vizuri, wawekewe misingi ambayo itawasaidia maisha ya mbele zaidi watoke hatua moja na kwenda hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwenye miji yote mikubwa hii, kama ambavyo kwenye kitabu chenu mmesema, ukitoka miaka ya 1967 mpaka leo kuna zaidi ya ongezeko la watu zaidi ya milioni 13 tafsiri yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko hili linapatikana kubwa sana kwenye miji. Kama hatutalitengenezea mkakati endelevu wa kudumu tutakuwa tunacheza mark time na hatuwezi kuwasaidia wananchi hawa. Kwa hiyo, ningependa sana tuone mkakati wa wafanyabiashara ndogondogo kwenye nchi hii inakuwa ni endelevu na mazingira yao tunatafakari namna ya kuwasaidia ili waweze kuendelea kufanya biashara zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni mpango wa kuzifanya Halmashauri ziwe na uwezo wa kukusanya mapato. Sote tunafahamu kwenye mpango hapa tumeshaanzisha sheria ambazo zipo, zilikuwepo na nyingine tumezihuisha sasa hivi, namna ya ukusanyaji wa mapato mengi na makubwa yaende kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Hili sio jambo jipya toka mwaka 2005/2006 lilifikiriwa, lakini halikufanyiwa kazi, mkakati wa upangaji wa matumizi asilimia 30 na 40 tunayoizungumza sasa hivi tunafahamu, ziko kodi zinaondoka kwenye Halmashauri zinakwenda kwenye Mfuko wa Serikali Kuu ikiwemo kodi ya majengo, ikiwemo kodi ya mabango na kodi nyingine kama tunavyoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni lazima tutengeneze mkakati kwenye mpango tunaoutazamia kuziwezesha Halmashauri zote nchini ziwe na uwezo wa kuanzisha vyanzo vingine vipya vya mapato. Kwa mfano, watu wanafikiria kujenga stand za mabasi, watu wanafikiria kuwa na miradi ya masoko ambayo inaweza ikaleta fedha nyingi kama kodi, lakini wapi wanapewa fursa ya kufanya hivyo? Hii PPP tunayoizungumza inaanza kufanya kufanya kazi kwa wakati gani na msingi wake ni upi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tujenge msingi ambao utasaidia kuhakikisha kwamba, suala hili Halmashauri zinakuwa na uwezo. Mbali ya fedha hizi zilizoondoka, lakini nzina uwezo wa kujiendesha, zitapata fedha ambazo Madiwani watafanya vikao, Wenyeviti watalipwa na mambo mengine kadha wa kadha yataendelea, lakini Mheshimiwa Waziri wa Mipango hujalizungumza humu ndani. Ninaomba ulichukue na utakapoleta mpango kamili tuone namna ambavyo Halmashauri zimewekewa mkakati, ili ziweze kusimama na kujitegemea zenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne naomba niizungumzie sekta ya afya. Sote tunafahamu kwenye sekta ya afya mipango tuliyopita nayo, kwenye mwaka 2015/2016, 2016/2017 na 2017/2018 tuliweka mkakati wa kuhakikisha kila Wilaya kwenye kila Kata na Kijiji tunakuwa na zahanati na vituo vya afya. Kwenye Mpango huu nimejaribu kuangalia naona tumejikita kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa,Hospitali za Rufaa za Kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina tatizo na hili, lakini lazima tufahamu kama tunashindwa kujenga vituo vya afya na zahanati za kutosha, kesi tunayoizungumza ya kuokoa maisha ya mama na mtoto hatutafanikikiwa kama tuta-base kwenye hospitali za Kanda peke yake. Sasa ni lazima tukubaliane tunapozungumza namna ya kumsaidia mama na mtoto wasiendelee kupoteza maisha, tumeongeza dawa kwa kiwango kikubwa lakini lazima iendane na ujenzi wa zahanati na vituo vya afya kwenye kata na vijiji vyetu, ili tuweze kuwa na msingi imara. Tunapozungumza kumuokoa mama na mtoto tuwe tunamaanisha kutokana na haya ambayo tunayafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumzia hospitali za rufaa. Hospitali za Rufaa tumeona ujenzi unaendelea, lakini mikakati ya kuboresha, humu imetajwa Benjamin Mkapa, imetajwa Hospitali ya Ocean Road, zimetajwa hospitali nyingine ikiwemo na Muhimbili. Pia, nishukuru kwamba mmesema jengo la wodi ya mionzi kwa ajili ya ugonjwa wa kansa pale Hospitali ya Bugando limeshakamilika na ni kweli, lina mashine kubwa za kisasa zinafanya kazi na gharama yake ni kubwa. Mpango mkakati wa kujenga jengo la wodi ya wagonjwa ni upi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwepo bajeti miaka mitano iliyopita. Kila mwaka unawekwa mpango haukamiliki, unawekwa mpango haukamiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninakuomba ukienda pale Ocean Road kwenye asilimia 100 ya wagonjwa asilimia 60 ya wagonjwa wa saratani wanatoka Kanda ya Ziwa. Sasa ni lazima tufikiri namna ya kuiwezesha hospitali yetu ya Bugando ili iwe na uwezo wa kujisimamia tukihakikisha kwamba tunapeleka fedha kwa ajili ya kutengeneza na kufanya ukarabati wa vifaa hivi, lakini bila kusahau ujenzi wa jengo la wodi ambalo litatusaidia kuepukana na matatizo haya ambayo tunadhani tukifanya vizuri yanaweza yakatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze juu ya habari ya miundombinu. Umezungumza juu ya habari ya miundombinu na focus yetu kubwa ni kwenye TANROADS. Lakini nikushukuru kwenye kitabu chako umesema, japo kwa uchache sana umeitaja TARURA kama chombo mbadala kinachokwenda kutatua tatizo la ardhi mijini na vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kutatua tatizo la barabara Mijini na Vijijini. Kazi wanayokwenda kufanya sasa hivi hawa TARURA moja ya kazi wanayokwenda kufanya sasahivi kubwa, uko mradi wa TSCP, uboreshaji wa Miji na Majiji kwenye Manispaa miji karibu Nane nchi nzima. Wana fedha nyingi zaidi ya shilingi bilioni 183 kujenga barabara kilometa nne, kumi, kulingana na mji wenyewe jinsi ambavyo ulivyo, lakini mkakati wa kuifanya TARURA kiwe chombo chenye nguvu, kiwe chombo ambacho leo hata Mbunge anayehudhuria kwenye Baraza la Madiwani kinapokwenda kutoa taarifa na yeye ajue, leo katika wigo wa Halmashauri hakuna sehemu yoyote Halmashauri inatoa taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa lazima tuzungumze pamoja. Kwenye mkakati tulionao TARURA kama ni chombo kitakachotusaidia, mkakati wetu ni nini wa kukifanya chombo hiki kiwe na uwezo, kiwe na fedha, lakini sisi ambao tunahangaika na barabara za wananchi tupate nafasi ya kuhoji na kujua ni nini kinachofanywa na kazi yake inafanyika wakati gani, ili tuweze kushauri, tuweze kusaidia na tujue umuhimu wa chombo hiki. (Makofi)

Mwisho tuliongelea bajeti iliyopita iko Mikoa iliyotajwa maskini, ukiwemo Mkoa wa Mwanza, Kagera, Mara, Singida na mingine. Moja ya kitu ambacho kimenishangaza sijaona mkakati wowote kwenye kitabu hiki unaozungumzia namna ya kukuza na kuondoa umaskini kwenye Mikoa hii.

Sasa utakapokuja na taarifa kamili kwamba, huu ndiyo mpango, Mheshimiwa Mpango naomba tuone ni namna gani tumejipanga kupunguza matatizo na kuondoa umaskini kwenye hii Mikoa mitano ambayo zaidi ya Mikoa minne iko Kanda ya Ziwa, tunafanya nini kuhakikisha kwamba, tatizo hili linaondoka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, lakini sio mwisho kwa umuhimu kama muda utakuwa unaniruhusu ni suala la viwanda. Serikali tunaipongeza sana kwa kuamua kuchukua Shirika la National Milling ambalo lina vipuri vyake karibia nchi nzima maeneo mbalimbali. Sasa ni lazima tujue mkakati wa Serikali kwenye hizi National Milling, pamoja na kazi kubwa itakayofanya kununua mahindi na mpunga kuyaongeza thamani kwa kuyasaga, na mimi nimshukuru sana Mheshimiwa Jenista hapa, kwa namna ya kipekee kabisa walivyofikiria hii mifuko ya jamii kuwekeza fedha huku ambako zinakwenda kuonesha tija kwenye hawa watu ambao wanashughulika na haya.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini tukisimamia vizuri ajira kwa vijana zitapatikana, lakini wakulima wanaolia leo watakuwa na sehemu ya kupeleka mazao yao. Wakiyauza yanasagwa yanatengenezwa yanaongeza thamani na tunaona umuhimu wa Serikali hii kuwahudumia Watanzania hawa wakulima na wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwa namna ya kipekee kuanzisha mpango wa kurasimisha ajira zisizo rasmi kwa vijana, ikiwemo kuwaongezea uwezo, kuwawekea ujuzi na stadi za kazi, ni idadi kubwa sana ya vijana, zaidi ya vijana 3,400 wako kwenye vyuo mbalimbali ikiwemo Don Bosco na TIA. Tunaamini vijana hawa wakikamilika na mpango wa vijana milioni nne kufikia mwaka 2021, tunaweza kuwa tumefanya jambo la maana kama mipango yetu inavyozungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na mwisho tu niseme jambo moja kwamba, tuko hapa kwa ajili ya kujenga nchi yetu, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kambi ya Upinzani, leo amezungumza vizuri na hivi ndivyo tunavyotakiwa tuseme, kwa sababu lengo letu ni kujenga nchi moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Mungu akubariki. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuzungumza juu ya hali halisi ya bajeti yetu ambayo tunaitegemea na Watanzania wengi sana wanaitegemea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende moja kwa moja kwenye mada kutokana na muda. Cha kwanza naomba niwashukuru sana watu wa Wizara ya Maji. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuangalia umuhimu wa kutoa kodi kwenye dawa zinazotibu maji kwa sababu kuondoa kodi hii kunazisaidia sana Mamlaka za Maji kuweza kutekeleza miradi yao midogo midogo kwenye kila eneo ambapo wapo. Hata hivyo, kutoa kodi kwenye dawa peke yake haitoshi, tungetamani sana na vifaa vinavyohusika katika shughuli za utengenezaji wa maji kama mabomba, pipes na nuts na vitu vingine ambavyo vinafanana na hivyo viondolewe kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili tumezungumza juu ya kujenga vituo vya afya na zahanati na huu ndio msimamo wa Serikali ya Awamu ya Tano. Hata hivyo, ingependeza sana tuseme tutajenga vituo vingapi na kila Halmashauri ijue tutaipa vituo vingapi ambapo mwisho wa siku tutafahamu tunao wajibu kwenye kila Halmashauri kujenga vituo vitano, kujenga zahanati tatu na kadha wa kadha, kama ambavyo tunaona Wizara ya Maji na Wizara ya Miundombinu wameelekeza vyanzo vyao kwa namba.
Mheshimiwa Naibu Spika, tungetegemea sana namba hizi kwani zingetusaidia kwa sababu tunatambua tunayo sera ambayo inasema kila zahanati inapojengwa kuwe na wakazi wasiopungua 10,000, tunafahamu iwe na umbali wa kilometa zisizozidi 10 lakini leo tunataka kujenga vituo vya afya kwenye kila Kata. Vituo vya afya hivi tunafahamu ni sawa na hospitali kwa sera ya sasa inavyotaka, ni lazima kuwe na OPD, ni lazima kuwe na maternity ward, ni lazima kuwe na ward ya wanaume na wanawake. Tutavijenga kwa mpango upi, kila Halmashauri itawezeshwa kwa kiasi gani, kuhakikisha vituo hivi vinajengwa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine ni juu ya kodi ya usajili wa bodaboda. Tunafahamu kwamba kodi hii inamhusu mtu anayeingiza pikipiki hii nchini, lakini huyu anapokwenda kuinunua bado hamjatoa maelekezo vizuri kule kwenye Halmashauri. Mngeelekeza vizuri kule kwenye Halmashauri, ziko kodi za leseni wanazotakiwa kulipa watu wa bodaboda hawajawahi kulipa hata shilingi moja. Sababu ni nini? Hakuna maeneo sahihi ya kuwapanga na kuwaelekeza kwamba hivi ndivyo vituo vyenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mtu wa bodaboda yenye magurudumu mawili anapaswa kulipia leseni Sh. 22,000, mwenye gurudumu tatu analipa Sh. 23,000. Uliza Halmashauri yoyote haijawahi kulipwa fedha hii kwa sababu Wakurugenzi wamekuwa wagumu kutenga maeneo ambayo yatasaidia sana kuhakikisha kodi hii inalipwa. Ukichukulia Mkoa wa Mwanza peke yake, kuna bodaboda zisizopungua 18,000 mpaka sasa hivi, kwa Sh.22,000 unapoteza zaidi ya shilingi milioni 396. Sasa tukiangalia haya tunaweza tukaona namna gani tunaweza kuwasaidia vijana hawa pamoja na gharama zingine ambazo zinaongezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunazungumza juu ya shilingi milioni 50 kwenye kila kijiji, wengine tunakotoka sisi kuna mitaa, tumeizungumzia vipi hii mitaa? Nimshukuru kwa kugundua Mikoa mingi ya Kanda ya Ziwa maana katika mikoa mitano, mikoa minne yote inatoka Kanda ya Ziwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najiuliza ikabidi nifanye utafiti kwa nini Mwanza tunaitwa maskini, kwa nini Kigoma wanaitwa maskini lakini nikagundua kulingana na idadi ya watu wengi tulionao Kanda ya Ziwa, umaskini wa watu wetu, watu wenye kipato kikubwa ni wachache na watu wenye kipato cha kati ni wachache na maskini ndiyo wengi zaidi kuliko maeneo mengine. Kwa sababu mmelijua hilo tungetamani sana tuone tunasaidiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mwanza uwezo wetu wa umaskini ni asilimia 35, Mheshimiwa Waziri ameongelea Geita umaskini uko kwa asilimia 48 na Kagera ni asilimia 43 na mikoa mingine. Sasa hizi shilingi milioni 50 tunazozizungumza tungetamani sana zianzie mikoa hii maskini, kwenye mitaa ili watu wake walioonekana kuwa na umaskini mkubwa waweze kusaidiwa na waweze kujikwamua na wao angalau wasogee kwenye kipato cha kati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunazungumza suala la kuhamisha kodi ya majengo kutoka kwenye Halmashauri kwenda kwenye TRA, iko mifano mingi. Mwaka 2007 walijaribu Dar es Salaam ikashindikana na leo tunarudi upya. Pamoja na sheria nyingi ambazo amezitaja humu ndani lakini Mheshimiwa Waziri hajatuambia kama anakumbuka Halmashauri hizi kupitia TAMISEMI Tanzania Bara na Ofisi ya Rais Zanzibar (TAMISEMI) ziliingia mkataba mwaka 2006 na World Bank (GIZ) na kupata fedha nyingi na malengo ya fedha zile ilikuwa ni kuboresha Miji, Makao Makuu ya Miji, Manispaa na Majiji na zimefanikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukipitia mradi wa TSCP, ukienda Mwanza, Mbeya, Arusha, Kigoma utaona haya ninayoyazungumza. Pia wameenda mbali zaidi wakaziwezesha Halmashauri hizi kupata fedha na kutengeneza mfumo wa GIS ambao umesaidia watu wamepewa mafunzo, wameelimisha watu, kwa ajili ya kuhakikisha wanapata data za majengo yote kwenye kila mji, leo tunakwenda kuondoa hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na sheria hizi alizozitaja, tunasahau iko Sheria Na. 2 ya mwaka 1983 inazozitambua mamlaka hizi za mitaa kwamba ndiyo mamlaka pekee zenye haki ya kukusanya kodi ya majengo. Hatukatai, inawezekana ninyi mmekuja na mfumo mzuri zaidi ambao sisi hatujui lakini kama Halmashauri na sisi kama wadau tunafahamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Halmashauri hizi zimeingia kwenye mikataba mikubwa hii tunayoizungumza, zimepewa vifaa kwa ajili ya kuboresha ukusanyaji wa taka, zimepewa vifaa kwa ajili ya kutambua majengo yaliyopo na thamani yake, kuondoa kodi hizi hawaoni kama ni athari kwa Halmashauri hizi? Ni lazima watuambie vizuri lengo na makusudi ni nini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, limezungumzwa hapa suala la kumpunguzia uwezo, mimi naita kumpunguzia uwezo CAG. Nilipokuwa nasikia michango ikabidi nitafiti zaidi, lakini Mheshimiwa Waziri atagundua mwaka huu wa fedha unaokwisha tulikuwa tumempangia CAG shilingi bilioni 74 ukijumlisha na fedha za wadau wengine alipaswa kuwa na shilingi bilioni 84. Mpaka tunavyozungumza CAG kapata shilingi bilioni 32 peke yake na maeneo aliyoyakagua ni ya matumizi peke yake, maeneo ya mapato ameshindwa kukagua.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kashindwa kufika kwenye mikataba mingi ya mgawanyo wa rasilimali za Taifa kama gesi kwenye madini na kadha wa kadha. Katika maeneo 27 ameenda maeneo sita peke yake. Leo tunamtengea shilingi bilioni 44 out of 74 ya mwaka huu unaokwisha, je, hawezi kupata shilingi bilioni 22 chini hata ya zile alizozipata mwaka huu? Hili ni lazima tuliangalie. Inawezekana wao wameliangalia vizuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tusitafakari vibaya, ni lazima tuhakikishe maeneo tunayotaka yakaguliwe vizuri na sawasawa tujiridhishe. Huyu CAG ndiyo tunamtegemea sisi, ili TAKUKURU afanye kazi yake vizuri anamtegemea CAG na ndiyo maana ata-Audit ripoti ya TRA mwaka huu imechelewa kwa sababu wamekosa fedha hizi, ni lazima tukubaliane tunachokiamua kiwe na maslahi kwa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa tunafahamu kwamba tunayo matatizo mengi. Tunazungumza viwanda lakini karibu miji yote nchini ardhi iliyotengwa kwa ajili ya viwanda siyo zaidi ya asilimia 2.5 na wakati matarajio na matakwa ni kuwa na asilimia 10 kwenye kila Halmashauri, ni wapi tumeweka?
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naomba niunge mkono hoja, lakini lazima tuangalie kinaga ubaga ni nini tunataka kuwatengenezea wananchi wa Taifa hili ili wafikie malengo ya Mheshimiwa Rais yaliyokusudiwa. Nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kwa kupata nafasi walau dakika tano hizi niseme machache ambayo nadhani yanaweza kutusaidia kuendelea mbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kuungana na mapendekezo ya Kamati zote mbili nikiamini kwamba ni moja ya maeneo muhimu sana ambayo kama Serikali itayafanyia kazi tunaweza kupiga hatua ambayo tunaitarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ninavyofahamu mimi suala la ukaguzi, katika Halmashauri zetu, Taasisi zetu na maeneo mbalimbali ambayo kwa kweli CAG anapaswa kufanya kazi huko zinasaidia kuimarisha utendaji bora na matumizi bora ya fedha za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamoja na uimarishaji huo, kama Kamati hizi mbili kama ambavyo zote zimesema haziwezi kupewa nguvu ya kufanya kazi ya kwenda field na kukagua kilichopo itakuwa bado ni sawa na kupiga mark time. Sababu moja kubwa ya msingi, kupata Hati Safi hakumaanishi yale yote yaliyofanyika yana ubora wa kiwango kinachostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana tunaamini kupata Hati Safi ni uandishi mzuri wa vitabu, lakini Kamati zinapokwenda field zinakutana na vitu tofauti; toka asubuhi Wabunge wameongea hapa. Sasa tunafikiri upo umuhimu, tunaamini kwamba, mambo haya yakifanyika vizuri sina shaka tutakuwa tumefikia malengo ambayo yametarajiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa zaidi, limezungumzwa suala la miradi kutokamilika kwa wakati. Naamini katika Halmashauri zote nchini miradi mingi sana ilianza. Hapa imetajwa miradi ya maabara, ikaja ya miradi ya vituo vya afya, zahanati, madarasa na kadha wa kadha. Vyote hivi, kama haviwezi kupelekewa fedha kwa wakati ni lazima tutakuwa tunakutana na hoja za ukaguzi mara kwa mara na hatuwezi kufikia malengo kwa kweli ambayo wananchi wanatazamia kuyaona sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Fedha za Mfuko wa Vijana na Wanawake; liko tatizo na mimi sina shaka Mheshimiwa Simbachawene atakuwa analifanyia kazi suala hili vizuri akishirikiana na Mheshimiwa Jenista kwa sababu moja tu ya msingi kwamba, fedha hizi imekuwa ni tabia, fedha hizi imekuwa ni mazoea, hazitoki kadri sheria inavyosema na Wakurugenzi wamefanya kama fedha hizi ni za miradi ya kwao pekee yao, si fedha za Serikali kwa mujibu wa sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, ningeomba uwekwe utaratibu tena ikiwezekana kwa maandishi kuisisitiza sheria hii kwamba ikiwezekana kila mapato ya mwezi yanayopatikana hata kama vitakuwa vinapata vikundi vitano mpaka 10, lakini mwisho wa mwaka watakuwa wana kiasi kikubwa ambacho wameshakitoa na itakuwa inaonesha uhalisia wa kile tunachokizungumza.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijana hawa ambao sisi tunaotokana na Chama cha Mapinduzi tumetoa ahadi nyingi na ahadi hizi kwa vikundi mbalimbali ambavyo vimeshaundwa kama haziwezi kutekelezeka bado tutakuwa hatuna maneno mazuri ya kuwaridhisha wananchi hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye Kamati ya PAC yapo mambo mengi hapa yamezungumzwa na muda uliopita huko nyuma tulisema hapa, kwamba pamoja na CAG kupisha bajeti ambayo tumeipitisha kwenye Bunge hili, lakini ipo miradi, kwa mfano ipo mikataba mikubwa, mikataba ambayo kipato chake tunaamini ni mgawanyo wa Taifa hili. Kwa hiyo kama hatutaweza, kwa mfano, mikataba ya gesi, CAG asipoweza kwenda kukagua huko na haya tunayoyaona bado hatuwezi kuona kile ambacho tunakitarajia miaka 10, miaka mitano ijayo katika kuhakikisha tunamsaidia Mtanzania huyu ambaye ni maskini sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni juu ya Kamati kushindwa kufanya kazi. Kamati hizi haziwezi kufanikiwa, Kamati hizi haziwezi kuleta matunda chanya kwa sababu kama nilivyosema, upatikanaji wa Hati Safi ni uandishi bora wa vitabu. Wako wahasibu mabingwa wa kuandika vitabu vizuri. Tutaendelea kusifia Hati Safi lakini miradi kule nyuma ni hewa, miradi haitekelezeki, miradi imekufa. Ni lazima tuhakikishe Kamati hizi zinakwenda kukagua miradi ambayo tunadhani imetumia fedha nyingi za Serikali na kodi ya wananchi pia katika kuhakikisha tunamsaidia Mtanzania huyu ambaye ni maskini na mnyonge.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kwa sababu ya muda; suala la PSPF, fedha nyingi bado hazijalipwa, tunafahamu Serikali imejiwekea mkakati wa kulipa zaidi ya bilioni 150…
Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru na naunga hoja mkono.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazofanya. Naishukuru sana Wizara kwa kutupatia gari la Ambulance kwa Kituo cha Lalago na Malampaka. Nashukuru sana kwa uzalendo wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa ninalotaka kuchangia ni kuhusu suala la waathirika wa madawa ya kulevya. Kama tujuavyo, kuna madhara makubwa ya kiafya kwa waathirika wa madawa ya kulevya (waraibu). Wizara ina jukumu la kupambana kuzuia baadhi ya madhara hayo ikiwemo maambukizi ya UKIMWI, homa ya ini (hepalitis B), TB na kadhalika. Moja ya shughuli ya kupunguza madhara haya ni pamoja na hatua za Serikali kupitia Sober House, lakini Wizara ina jukumu la kusambaza dawa ya Methodone na Syringe kwa waathirika (waraibu). Tatizo, Wizara haifanyi hivyo. Kuna upungufu mkubwa sana wa Methodone na Syringe. Syringe zinagawanywa na Wilaya moja tu; na Wilaya hiyo ni Temeke tu, Wilaya nyingine hakuna mgawo wa Syringe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, haioneshi juhudi maalum kwa waathirika hawa. Matokeo yake kundi hili linaathirika zaidi na wengine wanarudi kwenye utumiaji wa madawa hayo na wanapoteza maisha kwa magonjwa mengine nyemelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa mchana huu kupata nafasi kuzungumza kidogo juu ya habari ya Wizara ya Uvuvi na Mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kwanza kuzungumza juu ya habari ya mifugo ambayo Mwanza peke yake tuna kiwanda cha Tanneries. Moja ya viwanda vya mazao ya mifugo ambavyo kwa sasa havifanyi kazi na vipo ni pamoja na Kiwanda cha Nyama Shinyanga, Mwanza Tanneries na Kiwanda cha Maziwa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikuzungumza habari ya Mwanza Tanneries na nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mkuu wa Mkoa wangu wa Mwanza Comrade John Mongela kwa kazi kubwa aliyoifanya kuhakikisha kiwanda hiki kinarudi mikononi mwa Serikali. Miaka mingi kiwanda hiki watu wamekuwa wanapokezana tu hati na kuchukua fedha kwenye mabenki bila utaratibu wowote ili hali kiwanda kikiwa ni mali halali ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Mifugo kwa sababu yupo hapa wachukue jitihada na juhudi za haraka kuhakikisha viwanda hivi kwa kuwa vimerudi Serikalini vinapata wadau na vianze kufanya kazi haraka kwa sababu ndiyo malengo ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano kuhakikisha viwanda vinafanya kazi kwa maana ya Serikali ya viwanda na ajira zinapatikana kwa wingi. Pasi kufanya hivyo tutakuwa bado hatutimizi malengo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2015 - 2020 kuwasaidia Watanzania wengi na vijana kupata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye oparesheni Sangara. Operesheni Sangara, nitajikita hapo zaidi kwa sababu Sangara anapatikana katika Ziwa Viktoria peke yake. Ni ukweli usiopingika hakuna hata mtu mmoja miongoni mwetu anayepingana na zoezi zima la uvuvi haramu. Hata hivyo, nataka tu nijiulize mambo machache; tunapozungumzia uvuvi haramu leo lazima kuna watu ambao wanajulikana na shughuli yao kubwa ni uvuvi haramu peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka tu nijue na Wizara inisaidie kujua sana. Sangara hawa tunaowazungumza leo miaka ya nyuma ukija Dodoma hapa kwa kina Mzee Lubeleje walikuwa wanaletewa mapanki na vichwa. Leo Sangara huyu analiwa karibu nchi nzima akiwa nyama kama vile alivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu kujua leo tunapozungumza uvuvi haramu na zana haramu tunazozizungumza ni zipi? Tunazungumzia kokoro, timba, baruti, sumu au nyavu za inchi nne, sita na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Mheshimiwa Waziri kuna vitu viwili hapa, kuna wizara na kila wizara inapokwenda kwenye operesheni aidha inapotoka liko kundi lingine la uvuvi wa operesheni kutoka kwenye Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wavuvi wamenyanyasika sana, wako watu wanatumia jina la operesheni Mpina kwa sababu tu wakisikia Mpina ameingia wanatetemeka na wanatumia nafasi hii kuwaumiza sana wavuvi hawa kupitia jina lako. Natambua kazi inayofanywa na Wizara lakini yapo maeneo inawezekana wameyaacha wazi sana, wavuvi hawa wananyanyasika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano, nyavu ya macho 26, hii siyo haramu imeruhusiwa lakini wataalam wanajua na hata wao ukiwauliza nyavu hii tafsiri yake inavua kwenye maji madogo. Sasa kama inavua kwenye maji ya kina kifupi, nyavu hii ya macho ya macho 26 kwa nini isiende kutetekeza hicho kizazi tunachokitegemea, ombi langu turudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri alituma timu ya utafiti kutoka TAFIRI ikafanya kazi kubwa sana na wavuvi hawa. Chama cha Wavuvi wamezunguka takribani siku 14, wamekaa ziwani, wameangalia madhara ya nyavu yenye matundu 78 na matundu 52 na kujua tatizo lipo wapi, wameleta ripoti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri akiifanyia kazi vizuri ripoti hii itamsaidia na nyavu hizi zenye matundu 78 wanazoziita haramu na hapa mimi huwa najiuliza nyavu hii ina matundu 78, ukiipunguza mara mbili ukatoa moja ukatoa mbili inabaki 26 inakuwa siyo haramu, haramu haiwezi kuwa halali hata ukiigeuza vipi. Tuweke utaratibu mzuri ambao Wizara mnafanya na leo najikita sana kwenye kushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwanza tunayoiona leo nataka niwaambie haijajengwa na dhahabu na kitu kingine chochote, imejengwa na wavuvi hawa. Ukichukua ajira, ajira ya wavuvi wanaotega, wavuvi wamiliki wenye mitumbwi, ukachukua na ajira zilizopo kwenye viwanda, hawa wategaji na wavuvi wa kawaida ni wengi kuliko ajira za kwenye viwanda. Kwa hiyo, hii ni sehemu nyingine ya kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri tusimame sana, gharama za uvuvi zimepelekea wachuuzi wa bidhaa za uvuvi zimekwenda juu. Leo imeongelewa hapa boya moja la Sh.200 sasa hivi linauzwa Sh.400, lakini ukizungumza kamba iliyokuwa inauzwa laki moja na nusu, leo ipo mpaka laki mbili na themanini. Ni kwa sababu watu wajanja wachache wanatumia mwanya huo wa operesheni kujinufaisha wao na kuumiza wavuvi. Lawama zote zinazopigwa leo zinarudi kwenye Serikali ya Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, nataka niombe Mheshimiwa Waziri ashughulike na watu ambao hawataki kututendea mema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti uliofanywa unaonesha kabisa kwamba ziko aina ya nyavu hazina madhara kama zitatumika kuanzia kwenye maji ya kina kirefu na maeneo mengine kwa sababu nyavu hizo zinaonekana zinawasaidia watu hawa. Ukirudi leo ukizungumzia masuala ya faini ambayo watu wengi kweli wamepigwa faini na nimekuwa najiuliza, akitoka Mheshimiwa Waziri, kinaenda chombo kingine kinakwenda kufanya operesheni ya Wilaya na hiki ndicho kinachokwenda na ubabe wa hali ya juu, haujawahi kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitoe mfano, mtu ameenda kwenye kisiwa kimoja Goziba au Ilubwa kule akaenda kuvua amekaa kule siku 16 anasubiri samaki, ameondoka na barafu kutoka kwenye kiwanda Mwanza, amesafiri siku nzima kesho yake amefika ameanza kusubiri kununua samaki. Siku anarudi na samaki wake ameweka barafu, ile barafu kwa pale juu kadri ya siku alivyokaa inaanza kuyeyuka kushuka chini polepole, akikutana na Afisa Uvuvi kule ziwani anamwambia mbona barafu hakuna samaki ameonekana mgongo, anapigwa faini na anapewa masaa 24. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watu hawamtakii mema Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya. Naamini kazi hii ikifanywa kwa weledi mzuri na style nzuri baada ya miezi michache ijayo Mwanza tunazungumza dhahabu ya pamba itakuwa Ziwa Viktoria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi unawezaje kumpiga faini mtu ambaye unaona tu mgogo wa samaki umeelea juu, kwa sababu barafu imeyeyuka. Mtu huyu akifika kiwandani hakuna Sangara anayeoza, akifika kwa mwenye kiwanda, mwenye kiwanda atachukua samaki anaowataka. Wale wengine ndiyo maana wanatengeneza kayabo, wanakwenda kuuzwa nchi za jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niwaombe sana Maafisa wa Uvuvi wawe wanaangalia na wao ni wataalam wanajua misingi thabiti ya jambo hili kubwa wanalolifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ninalotaka kuchangia, Mji wa Mwanza biashara zake zote, kwa mfano leo dizeli haiuzwi, petroli haiuzwi kwa kiwango hicho kwa sababu wenye mahitaji haya ni hawa hawa. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri na jambo lingine kubwa tufanye mkakati kama Wizara na Serikali, tumekuwa tukifanya sana huko na tumesikia asubuhi hapa masuala ya bahari kuu vinatafutwa vifaa vya uvuvi na kadha wa kadha kwenye bahari kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri hapa amejibu vizuri, lakini hebu tujiulize wavuvi wa Kanda ya Ziwa wanapokwenda ziwani kuvua wanatumia fikra zao, wanabuni, wanahisi sehemu fulani leo kunaweza kuwa na samaki wengine wanaweza kuwa wanafuata mwezi, wanahisi au wanaweza kuwa wanabashiri ni wapi samaki watapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yake Waziri, Mheshimiwa Mpina itengeneze sasa utaratibu, ifikirie mpango thabiti wa kuwasaidia wavuvi wa Kanda ya Ziwa ili na wao wawe na vifaa; wanapokwenda kule kwenye maji wawe na uhakika nakwenda na nyavu yenye matundu kadhaa, ninapokwenda kutupa nyavu ndani ya masaa sita nitakuwa nimepata samaki ninaowahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wavuvi hawa anaweza kuwasha boti kutoka kwenye kisiwa akafika mpaka ziwani, akaishia kilo mbili amechoma mafuta ya gharama akarudi akakutana na operesheni hata zile kilo mbili akanyang’anywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, yeye bado kijana ana uwezo mkubwa wa kufanya kazi hii na akabaki kwenye historia kukumbukwa kwenye Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hivi tunavyokwenda Wizara inaweza ikatusaidia sana kuhakikisha wavuvi na wafugaji katika Taifa hili wanabaki salama, lakini anaanzsiha vitu ambavyo vitakuwa na historia kubwa, vitamjenga ataacha legacy kwa wavuvi hawa. Mheshimiwa Waziri asimamie watendaji wasiokuwa waaminifu wanaendelea mpaka kesho. Leo wanasema ukifika kwenda kukamata operesheni kabla hujakamatwa umeona boti, unatupa kwanza bomu na hii imetokea na taarifa ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, tusimame kwenye misingi ya kulisaidia Taifa hili. Narudia tena miezi michache ijayo Ziwa Viktoria itakuwa na dhahabu ya pamba kama hatutawanyanyasa watu hawa na kupora mitaji yao kwa namna ambavyo inatupelekea kubaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. STANSLAU S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushuru kwa kunipatia nafasi hii jioni ya leo kuchangia kwenye bajeti hii muhimu kabisa kwa ajili ya wananchi wa Tanzania. Pia niungane na Waheshimiwa wote ambao wamepata nafasi ya kuchangia lakini ambao wameona umuhimu wa kuendelea kuishukuru Serikali na kuipongeza kwa kazi kubwa ambayo imeendelea kuifanya katika kuhakikisha inatatua changamoto za Watanzania. (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yetu ni kwamba bajeti hii ya mwaka 2018/2019, pamoja na muonekano wake wa kwamba inakwenda kujibu changamoto nyingi ambazo tumekuwa tukizijadili kwenye miaka mingi iliyopita, lakini yako mambo ambayo ni lazima sasa tuendelee kuyazingatia. Kwa sababu tumeamua kuyaleta sasa ni lazima tuyasimamie ili utekelezaji wake ukaonekane moja kwa moja kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ameongelea suala la uimarishaji wa viwanda vidogo kwa maana ya SIDO lengo lake likiwa ni moja tu kubwa kuendelea kutoa ujuzi na taaluma mbalimbali kwa vijana ambao hawajafikia kiwango kikubwa cha elimu ili wawe na ujuzi ambao utawasaidia katika soko la ajira hasa tunapokuja kuzungumza habari tarajiwa ya viwanda vingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo la viwanda vya SIDO au wazo la hivi viwanda vidogo vidogo lazima liwe na mipaka. Inawezekana sana tunakosea; leo unakwenda kule kwa kina Mzee Lubeleje kijijini kabisa kule au kwa kina Mzee Mwamoto kule nako unataka kuweka kiwanda cha SIDO watu wengine wamezoea shughuli tu za kulima wanataka walime tu. Kwa hiyo nimwombe sana tuangalie, tuwe na malengo. Inawezekana tukachukua manispaa, halmashauri za miji na majiji tukaimarisha shughuli za viwanda vidogo vya SIDO kwa kuanzia ili tuzalishe wataalam wengi zaidi na kuzalisha vifaa vingi zaidi ambavyo vitasaidia kuvipeleka ma mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nizungumzie juu ya habari ya wazabuni. Mheshimiwa Waziri ni shahidi wamekusanya fedha nyingi sana na Serikali imefanya kazi kubwa sana. Wazabuni waliofanya kazi na taasisi za elimu, shule, hospitali na maeneo ya taasisi za Jeshi la Polisi na wananchi wanapata tabu sana ya malipo yao kwa muda mrefu sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwaomba sana tujitahidi kwa namna yoyote ile tuhakikishe tunalipa madeni haya, kwa sababu kwa kuwalipa hawa tunaongeza mzunguko wa fedha. Naamini Mheshimiwa Waziri fedha tunazo nyingi sana za kutosha na baadaye nitamwambia kwa nini fedha hizi naamini anazo kwa sababu ya mambo makubwa ambayo Serikali hii imeyasimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kodi ya ardhi; Mheshimiwa Kishimba hapa amelizungumza na mimi niliseme kwa namna ya tofauti kidogo. Niwashukuru sana Wizara ya ardhi kwa kuamua kuanzisha urasimishaji wa makazi kwenye miji yote mikubwa. Maana yake ni nini, kodi tunayokusanya sasa naamini kodi ya ardhi haijafikia hata asilimia 30. Tukiweka mfumo mzuri majengo yote ambayo tunataka yapimwe yakapimwa sawasawa, naamini Serikali hii kupitia kodi ya majengo peke yake Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango anaweza akakusanya fedha nyingi sana na zikaendelea kutusaidia katika kutatua changamoto tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivi hatutakuwa leo tunahangaika kuwa na bajeti ambayo mwisho wa siku hatufikii malengo ya ukusanyaji wa fedha. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, naamini, leo kila mtu anashangaa kwa nini Serikali inafanya miradi mikubwa, lakini ukiangalia fedha peke yake tunayokusanya kwa mwezi mmoja na matumizi tulioyonayo hayalingani na kiasi tunachokusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Mheshimiwa Mpango anasahau naye kwenye hotuba yake amemsifu sana Mheshimiwa Rais, lakini naona amemsifu kwa vitu vidogo vidogo sana. Nimkumbushe Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango, wakati najaribu kusoma kuangalia, miaka ya nyuma huko wakati sisi tuko nje tunatamani kuja kwenye Bunge hili tulikuwa tunaona Bunge likisimamia na kulalamikia mambo makubwa. Leo tumekuja humu mambo haya yote yamefanyiwa kazi na Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Mpango hajatuambia kwa mfano wako Wabunge humu mwaka 2012/2013 alikuwa Mheshimiwa Mpina, Mheshimiwa Ndugulile na wengine wengi walifika hatua ya kugomea bajeti hii kama hii tunayoijadili leo wakitaka mambo ya msingi ambayo Serikali iilkuwa inashindwa kuyasimamia wakiamini yangeweza kuleta mapato mengi kwenye Serikali lakini yalishindikana. Leo Mheshimiwa Dkt. Mpango tunazungumza hapa, nimpe mfano wa mambo matatu tu kwa haraka haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi si Mhasibu lakini nilikuwa nasoma naona, wanazungumzia habari ya illicit financial flows; yeye anafahamu kwa kiasi gani Serikali ya Awamu ya Tano imezuia masuala yote yanayotokana na mfumo huu. Haya ni pamoja na mikataba ya kampuni nyingi ambapo mikataba ya kampuni zinazoshughulika na rasilimali za Taifa zilikuwa zinasimamiwa na zilikuwa zimeachwa wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mpango ni shahidi, hapa wamesimamia masuala ya mikataba, masuala ya usafirishaji wa mizigo. Kwa mfano mdogo alikuwa akija hapa tunasikia tunauza nguzo nje ya nchi, lakini zinauzwa hapa nchini zinapelekwa Kenya au south Africa halafu zinarudishwa hapa zinanunuliwa kwa gharama kubwa zaidi. Hili limekoma na limekwisha, leo ni kiasi gani cha fedha kimeokolewa hapa? Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri kuna kitu kinaitwa dollarization, matumizi ya dola nchini. Mtu alikuwa anaweza kuja na begi zake za dola akaondoka na begi zake za dola hapa hakuna mtu anauliza. Leo kwa kiasi gani Serikali yake imefaidika na kuzuia utaratibu wa matumizi ya dola yasiyokuwa na mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge hili mwaka 1992 Mheshimiwa Waziri wewe ni shahidi kwa kiasi kikubwa sana leo nchi yetu haiko kwenye mfumo wa matumizi ya moja kwa moja kwa dola kama Zimbabwe na nchi zingine. Sisi dola ni matumizi ambayo si ya lazima, lakini sheria iliyoruhusu kufunguliwa account za dola na matumizi ya dola imeweka mipaka ambayo ilikuwa wazi, leo wamedhibiti maeneo hayo na fedha zinapatikana kwa wingi; hii ni sambasamba na transfer pricing.

Mhehimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mambo haya makubwa ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imeyafanya yametuongezea fedha kiasi gani, yameiongezea Serikali nguvu ya kiasi gani, aje hapa awaambie Watanzania wajue mabadiliko ambayo Mheshimiwa Rais ameyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana tukisimama hapa tunaongelea Mheshimiwa Magufuli kafanya mambo makubwa watu hawatuelewi na ndiyo maana wanasema msisifie tu. Yako mazingira yanatulazimisha tusifie na Mheshimiwa Waziri anapokuja atuambie kwa kiasi gani Serikali imeokoa fedha nyingi kwenye maeneo hayo matatu na ambayo leo tunazungumza Serikali hii tunaweza kuwa na miradi mikubwa ambayo inafikirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwenye kila halmashauri tunazungumzia kujenga vituo vya afya, hospitali za Wilaya 60, tunazungumzia kujenga vituo vya afya kila kata, fedha zinatoka wapi? Tulizonazo ukipiga hesabu hazitoshi, lakini kwa sababu kuna mifumo wamesimamia, wamezuia fedha nyingi zaidi zimepatikana, ndio maana Serikali ya Awamu ya Tano ina fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie jambo moja dogo sana, tunazungumza habari ya mjadala hapa namna gani Serikali inataka kuanzisha Mfuko mmoja (Treasury Single Account); wala si jambo jipya. Tukifuatilia kwenye hotuba na mijadala ya Bunge la mwaka 2014 suala hili limepitishwa na maazimio ya Bunge hili bada ya umoja wa nchi za Afrika Mashariki na Kati kuamua kuwa na mfumo huo. Sasa leo hapa tunataka kulifanya kama jambo jipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ukichukulia kwenye halmashauri zetu, mwaka mzima uliopita leo kati ya halmashauri 151 tulikuwa na zaidi ya account 1,500, leo tuna account zisizopungua chache 150 na kitu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo nilikuwa kwenye pick sasa, naunga mkono hoja kidumu Chama cha Mapinduzi. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na mimi mchana huu nikiamini kwamba kazi tunayoifanya hapa ni kazi ya kuisaidia na kuishauri Serikali na kulisaidia Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe ya Kamati ya PAC, pamoja na mambo mengi yaliyozungumzwa lakini pia nasikitika kuamini kwamba na sitaki kuamini kwamba watu wanatamani kusikia mabaya siku zote, lakini wakati unakumbuka kusikia mabaya lazima tukubaliane na hili wala halina ubishi na mazuri yapo na kazi hizi zinafanywa na binadamu. Kama zinafanywa na binadamu hakuna mwanadamu aliye mkamilifu katika nchi hii au dunia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachotaka kusema CAG kwa mara ya kwanza amefanya kazi kubwa sana na ninyi ni mashaidi wakati tunaingia hapa tulilalamika sana suala juu ya kumuwezesha CAG kufanya kazi kwenye maeneo makubwa. Kwa mara ya kwanza CAG hajakuwa na malalamiko ya kibajeti kwa mwaka wa fedha ulioisha na kazi kubwa sana aliyoifanya. Yeye mwenyewe amedhibitisha, kati ya mashirika 200 aliyotazamia kukagua amekagua mashirika 188, lakini taasisi za Serikali pamoja na taasisi zingine alipanga kukagua taasisi zaidi ya 241 na zote hizo amezikagua kadri alivyoweza na kwa nguvu zake zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ukaguzi huu kama nilivyosema haiwezekani watu hawa wote wakawa malaika, lakini makosa ya kibinadamu yanakuwepo. Mimi niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati na Mwenyekiti wa Kamati, mmefanya kazi kubwa na kwa utulivu mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nijikite tu kwenye hoja kama tatu hivi; cha kwanza cha kwanza ni ration za polisi ni aibu sana na mimi nimuombe kwa sababu Mheshimiwa Kangi yupo hapa ripoti karibu zote tunazozizungumza humu ndani, Mheshimiwa Halima alisema kwamba ripoti moja tu ndiyo ilikuwa ya ukaguzi maalum, tuna ripoti takribani nne ni ukaguzi maalum kwenye taarifa tunayoisoma hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala ration za polisi Mheshimiwa Waziri yupo hapa, maana humu tunaweza tunahangaika, kila mmoja amekariri jambo moja, anataka aseme hilo hilo apotoshe afurahi aendelee mbele. Fedha zaidi ya bilioni 888 zimelipwa kwa watu wasiokuwa maaskari wakati askari wetu wanahangaika awapati ration kwa wakati Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Jambo hili limekuwepo muda na hakuna mtu anayechukua hatua hata mmoja. Tukuombe sasa Mheshimiwa Kangi tunataka watu hao wapatikane, wachukuliwe hatua na fedha za umma zilizotakiwa kwenda kwa wahusika zipelekwe, vinginevyo tutabaki hapa tunalaumiana tunapiga kelele alafu atuendi kwenye mambo ya msingi ambayo tunataka yawasaidie Watanzania, ni lazima tuhakikishe mambo haya yanafanyiwa kazi na yanapata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nigusie kidogo suala la NSSF. Inawezekana kabisa watu waliokuwa wanafikiria, walifikiria vizuri, lakini wale waliokuja kutenda wametenda kinyume na mipango iliyokuwa imetengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano tumezungumza hapa na sisi tumeangalia upande mmoja tu hapa, tumeangalia upande wa ardhi ambazo zilikuwa zinanunuliwa kwa ajili ya kuhifadhi kwa matumizi ya uwekezaji. Uwekezaji ulikuwa wa aina gani? Mpango wa kuekeza ulikuwa ulikuwa upi? Feasibility study ilifanyika kwa kiwango gani? Yote haya hayakuonekana. Hapa tunazungumza ukienda Mwanza, ukienda Arusha, ukienda Dar es Salaam, ukienda sijui Pwani, kila sehemu ni matatizo matupu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano fedha iliyonuniliwa ardhi peke yake ni zaidi ya bilioni 27. Shilingi bilioni 27 inaponunua ardhi tafsiri yake ni nini, lazima tuwe na mipango madhubuti ambayo tulielekeza kule. Hizi taasisi sio kwamba hazikuwa na watu au zilikuwa hazisimamiwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikupe tu mfano mmoja mdogo ukichukua pale wanasema mfano ukienda Dar es Salaam wanasema wamenunua ardhi Dar es Salaam na Pwani kwa zaidi ya shilingi bilioni 14 plots tano, zinatajwa plots tano. Inaweza kuwa ya square mita 4,400, inaweza kuwa square mita 30 ama inaweza kuwa square mita 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninachosema hapa ni kwamba hatuwezi kuendelea kubaki tunalalamika. Mimi niishukuru sana Serikali kwa kuamua kuunganisha mifuko hii na kupata mifuko miwili. Sasa ni wajibu wa BOT na SSRA kuhakikisha mifuko hii haiingii tena kwenye mikataba ya hovyo itakayotupeleka taifa na watumishi wetu kukosa michango yao wanapohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo tutakuwa tumeisaidia Serikali tutakuwa tumelisaidia Taifa, lakini ardhi yote ambayo inaonekana ipo ipo juu ufanyike uhakiki wa kina sasa itambuliwe na Halmashauri zote zinazohusika zihakikishe hati ardhi hizi zinapatikana, vinginevyo tunapiga tu mark time tu hapa halafu hatuwezi kuisaidia nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Suala lingine ningependa nizungumzie NDC. Ni kweli NDC ni shirika la maendeleo ambalo limetengenezwa maalum kwa ajili ya kusaidia kwa haraka na kwa kazi uwekezaji kwenye sekta ya viwanda na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa mfumo wa shirika hili lilivyo, kama tutaendelea kuliegemea, nataka nikuahakikishie hakuna hata siku moja linaweza kuwa zao bora kwenye viwanda tunavyovitegemea na haliwezi kumsaidia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano limezungumzwa hapa TANCOAL na PCEA. TANCOAL tunafahamu ni taasisi au ni kampuni iliyoundwa kutoka Serikalini na hii inayoitwa PCEA ni mwekezaji aliyekuja, sasa cha ajabu kabisa uwezi kukifikiria TANCOAL imechukua asilimia 30 lakini hawa waliokuja kama wawekezaji wamepewa asilimia 70. Mtaji wa mwekezaji ni shilingi milioni 1.75. Moja ya makubaliano ni lazima atoe dola milioni 20 na dola milioni moja 1.47 zinunue vifaa na kuwekeza kwenye magari.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka mmoja baadae, mwaka 2012 mwekezaji kaenda kukodi vyombo na magari vyenye dhamani ya dola milioni 42.7. Tafsiri yake ni nini, mwekezaji huyu awezi kulipa kodi ya Serikali hata senti moja, hawezi kulipa mrabaha wa makubaliano ya Serikali, lakini zaidi ya yote kila mwaka kukicha kukirudi anapata hasara na hata walioingia mkataba Mheshimiwa Kiswaga hapa amesema hivi kweli tuna watu leo wanakaa kwenye ofisi hawezi kufikiria mkataba alioingia asilimia 70 na 30 anazobaki nazo kama Serikali hatujui hata dhamani ya mawe yanayokwenda kuchimba na kwa umri upi?

Mheshimiwa Naibu Spika, watu hawa wapo, wanaishi, wanakula maisha, hakuna hatua, tumekaa, bodi imeuliza maswali ya kutosha lakini imetumia muda muda mchache sana mpaka leo haijaleta hata jibu moja juu ya hii. Tuombe sana Serikali na Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji upo hapa, hili ndilo eneo sasa tunataka tumsaidie Mheshimiwa Rais anayefanya kazi kubwa ya kulinda rasilimali za taifa hili ya kuhakikisha tunafaidika na rasilimali zetu ya kuahakikisha tunapambana na mambo yote yaliyokuwa ya ovyo, kuisaidia Serikali irudi kwenye wakati unaofaa kwa ajili ya umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunafahamu na mimi nimesema sana, haiwezekani na haitakaiwezekani kila siku tukikaa hatuna suluhu, tunataka tufike sehemu. Leo tunasema Mheshimiwa Kangi kuna magari 777 hayaonekani na ninyi mpo. Tusaidieni haya mambo yashughulikiwe, tuondoe maswali kwa watu, tumwache Mheshimiwa Rais ashungulike na mambo ambayo yanaweza kulisaidia Taifa hili na kuweka maendeleo zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumza fedha zote tunazozisema hapa, pale Nyamagana ukija nahitaji Vituo vya Afya vitatu tu ninacho kimoja sasa hivi. Fedha hizi ni nyingi nahitaji barabara za lami kama kilometa 30 hivi. Fedha hizi zingeweza kusogezwa pale zikawasaidia wananchi na maeneo mengine mengi. Ndiyo, ananikumbusha kwa mfano ukiwa unatoka Nyegezi unaenda Majengo barabara ni mbaya kule, ingewezwa kutengenezwa kupitia hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nakushukuru sana na Mungu awabariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu kabisa katika ustawi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu kama Waheshimiwa Wabunge wengine, ambavyo wamempongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri ambayo kwa kweli inaonesha matumaini ya hili suala tunalolizungumza juu ya Serikali ya viwanda inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Rais kwa namna ya kipekee kwa kutambua umuhimu wa kuwa na viwanda ambavyo ndiyo unaweza kuwa msingi wa wakulima wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ufahamu huu tulionao wote, lakini pamoja na hii ambayo ndiyo kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais kwa sasa, bado tunayo kila sababu ya kuhakikisha vyuo vyetu vya VETA na mitaala tuliyonayo inatambua umuhimu wa Serikali hii au Taifa hili kuwa na viwanda ili viweze kuchukua sehemu kubwa sana ya vijana kama ajira lakini ya uzalishaji mali na mazao ambayo yatakuwa yanatumika zaidi kwa wananchi hawa wanyonge lakini na kuuza nje ya nchi kama ambavyo tunatarajia kupata kipato kikubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunatambua, nami leo nitajikita sana kwenye viwanda ambavyo, pamoja na utaratibu huu tunaoufikiria sasa wa kuwa na viwanda vipya au ujenzi wa viwanda vipya katika maeneo mbalimbali ya nchi hii lakini nataka nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba tunayo kila sababu viwanda hivi tunavyovijenga kwa sasa ni lazima tuwe na kipaumbele na viwanda tunavyovihitaji kwa ajili ya maslahi ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu muda wa miaka mitano ni mchache sana; tukisema miaka hii mitano tunaondoka na viwanda 100, 200, 3,000 au mia ngapi, bado tutakuwa tunajidanganya, tutakuwa na ma-carpenter wengi, hatutakuwa na SIDO nyingi halafu tunahisi tuna viwanda vikubwa ambavyo vinaweza vikasaidia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaona mfano; tunapozungumzia uhaba wa sukari nchi hii, tunazungumzia moja kwa moja uzalishaji hafifu wa viwanda vyetu tulivyonavyo hapa nchini. Pamoja na uhafifu huo, tunayo mifano; Kenya, Uganda na nchi nyingine zinazotuzunguka, nataka tufikirie kuwa na viwanda vyenye vipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uchache huu, leo Mheshimiwa Waziri anaweza akajinadi na ana kila sababu ya kujisifu; hata bei ya sukari tunayolalamika sisi iko chini, huwezi kulinganisha na nchi za majirani zetu kama Uganda na Kenya. Sasa maana yangu ni nini? Unapokuwa na viwanda vya sukari vyenye kuweza kuzalisha zaidi, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo tulikuwa tunazungumza naye pale, wamekamata sukari ya Kilombero inaingizwa Kenya kule kwa magendo; na sababu ni moja tu; inawezekana uhaba huu tulionao bado sukari yetu inavushwa nje. Sasa maana yangu ni nini? Nataka tuwe na viwanda vyenye vipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukiwa na viwanda yenye vipaumbele kwa miaka hii mitano, tutajikuta tunafanya kitu ambacho kitakuwa kinaonekana kwa Watanzania kuliko kubaki na historia ya ujenzi wa viwanda lukuki ambavyo havina vipaumbele kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine; nimesema mbali ya kuwa na viwanda vya kipaumbele, lazima sasa tuangalie, tunapiga hatua 100 mbele kufikiria viwanda vipya, tuna mawazo gani juu ya viwanda tulivyokuwanavyo toka zamani na leo tulivibinafsisha na haviwezi kufanya kazi yake sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Mwanza tunavyo viwanda vya Tanneries, tunacho kiwanda cha MWATEX lakini tunavyo Viwanda vya Samaki. Kiwanda cha MWATEX ambacho toka mwaka 1995 kilibinafsishwa, wafanyakazi zaidi ya 1,720 ambao waliachishwa kazi na mpaka leo hawajalipwa, lakini kiwanda kile pamoja na mambo yake mengi, hivi tunavyozungumza, uwezo wa kiwanda hiki kuzalisha hata asilimia 30 ya yale yaliyokuwa yanazalishwa miaka karibia 12 iliyopita, hakijafikia malengo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha MWATEX kila mmoja anafahamu, kila mmoja anajua umuhimu wa viwanda hivi; ni wakati gani tuko tayari kurudi kwenye viwanda hivi na tushughulike navyo viweze kuzalisha kama zamani? Mbali ya ajira kubwa ya zaidi ya watu 2,000, lakini vilikuwa na uwezo wa kuzalisha na tutasafirisha nje kwenye nchi za majirani na kwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeongelea Kiwanda cha Tanneries. Kiwanda cha Tanneries kimebinafsishwa. Kiwanda hiki sasa Mheshimiwa Jenista pamoja na Wizara yake wameanzisha mafunzo muhimu kutoka nchi nzima vijana wanapelekwa pale zaidi ya 1,000. Hawa vijana wakimaliza kujifunza pale wanakwenda kufanya kazi wapi? Kiwanda hiki tangu kibinafsishwe hakijawahi kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba na hiki na chenyewe tukiangalie. Hawa vijana wanaotoka DIT kwenye mafunzo ya utengenezaji wa mikanda, viatu na mikoba, kiwanda hiki ikiwezekana kama siyo kurudishwa; na Mheshimiwa Rais aliahidi, tuangalie uwezekano wa kurudisha kiwanda hiki kije; vijana wanaotoka kujifunza hawa badala ya kwenda mtaani, watakuwa wanazalisha mali zilizokuwa na ubora. Wafanye kazi kwenye kiwanda hiki, wazalishe mali zenye ubora, tuuze ndani na nje ya nchi kwenye majeshi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, ni viwanda vya samaki. Tuna viwanda saba vya samaki. Hii ni lazima Mheshimiwa Waziri akubali kuungana na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili waweze kuona. Miaka minne iliyopita kiwanda kimoja peke yake kilikuwa kinakata shift nne, watumishi zaidi ya 1,400, kikiwa kinakata tani 280 za samaki kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kiwanda kimoja kinaitwa Vicfish kimeshafungwa; na hivi vilivyopo kimoja kina uwezo wa kuzalisha tani sita mpaka 12 kwa siku, kimepunguza wafanyakazi kutoka 1,400 mpaka 300 mpaka
150. Tafsiri yake ni nini? Tunaongeza Machinga, tunaongeza wafanyabiashara ndogondogo, ajira hakuna na kumbe tunaweza kushirikiana tukatengeneza ajira nyingi zaidi kama viwanda hivi vinaweza vikaboreshwa upya. Kazi inayofanyika ni nzuri, lakini lazima tunapokwenda mbele tukumbuke na tulikotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mpango wa sasa, viwanda tutakavyovijenga Mwanza, vinategemea kuzalisha ajira 1,004. Hawa tunaozungumza viwanda vilivyokufa, zaidi ya ajira 2,900 zimepotea. Tafsiri yake, tunahitaji viwanda hivi viangaliwe upya na ushirikiano kati ya Wizara mbili au tatu ni lazima uwe wa karibu ili kujenga msingi wa viwanda tunavyozungumza viweze kufikia malengo yake tunayoyatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda lazima akubali kushirikiana. Watumishi hawa ambao miaka 12 hawapo, leo wapo mtaani, wengine wameshakuwa wazee, tunahitaji kujua ni lini watalipwa mafao yao ambayo hawajawahi kuyapata miaka 12? Tukifanya hivyo itatusaidia, tutakwenda mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. Mungu akubariki sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana nami kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii kwenye Wizara hii muhimu kabisa kwa maisha ya Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mungu lakini kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, pamoja na
watendaji wote wa Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Kiukweli Wizara hii pamoja na changamoto nyingi sana tulizonazo kwenye sekta ya ardhi, sina shaka wenzangu watakubaliana nami kazi kubwa sana imefanyika kwenye sekta zote; kupima, kupanga pamoja na kutatua migogoro mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuishukuru sana Wizara, nawe kama Mbunge wa Mbeya utakubaliana nami kwamba moja ya majiji yenye changamoto kubwa za makazi kwa wananchi na maeneo yake, Jiji la Mwanza ni kama ilivyo kwa Jiji la Mbeya. Namshukuru sana Mheshimiwa Lukuvi, Bunge la Kumi na Moja baada ya maombi ya muda mrefu alihamua kwa dhati kukubali Leseni za Makazi baada ya Dar es Dalaam ziende Mwanza, Arusha pamoja na kwako Mbeya. Sina shaka zoezi hili litafanyika na limeshaanza na inawezekana likawasaidia sana wananchi wa Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Mwanza unafahamu maeneo ya Mabatini, Pamba, Isamilo, Igogo na baadhi ya maeneo ya Mkuyuni, wananchi wote waliozunguka kwenye vilima, walikuwa hawana sifa hata ya kulipa kodi ya ardhi kwa sababu maeneo yao hayatambuliki. Leo naamini Serikali kwa mpango iliyonao wa kurasimisha makazi haya na kupata Leseni za Makazi zaidi ya kaya 15,000 tutakuwa tumeisadia Serikali na Wizara kupata mapato. Hii ndiyo moja kati ya kazi kubwa zilizofanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa taarifa tu, nitumie nafasi hii kuwapongeza sana watendaji wa Jiji la Mwanza wa Kitengo cha Ardhi, pamoja na changamoto, wanafanya kazi kubwa. Leo tuko zaidi ya nusu ya kazi ambayo Mheshimiwa Waziri umewaelekeza na wamekusudia kuifanya. Tayari tumeshatambua vipande vya viwanja hivi zaidi ya 9,437. Hii siyo kazi ndogo kati ya viwanja 15,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na niendelee kumwomba asituchoke, aendelee kutusaidia kwa sababu ndilo jukumu aliloaminiwa nalo; na bado Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Mama Samia ameendelea kumwamini. Sina shaka anafanya vizuri kwa sababu ana timu nzuri ya watendaji ambayo imesheheni pamoja na Naibu Waziri ambaye ni msaidizi wake, kwa karibu wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, napenda kuzungumzia suala la urasilimishaji wa makazi. Ni mfano ule ule tu, tumekuwa na changamoto kubwa zinazotokana na migogoro. Hii inawezekana ni kwa sababu maeneo mengi yalipimwa na kupangwa zamani. Kwa namna moja au nyingine kutokana na kukosa fedha na changamoto mbalimbali, maeneo haya hayakuendelezwa kwa wakati na badala yake wananchi walio wengi wakaingia kwenye maeneo haya. Sasa Serikali inapoteza kodi katika maeneo yote mawili; mtu aliyemilikishwa mwanzo hajaonekana zaidi ya miaka 30, wananchi wamejenga kwenye lile eneo, wameanza maisha yao, wamejenga majumba na maisha yanaendelea. Siyo rahisi sana kuvunja zaidi ya nyumba 200, 300 au 500 kwa sababu tu eneo hili alipewa mtu mmoja hati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amekuja Mwanza na Naibu Waziri amekuja kwa wakati tofauti, wamefanya kazi kubwa sana. Mifano iko mingi, ukienda kule Mandu Mtaa wa Sokoni, tumefanya maamuzi ambayo leo yametuweka kwenye hali nzuri ya wananchi waliokuwa wamepoteza matumaini na sasa wana imani kubwa na Serikali yao, chini ya Mheshimiwa Mama Samia wanaamini kwamba wataendelea kuijenga Serikali hii.

Mheshimiwa Naibu Spika na Mheshimiwa Waziri, bado tunayo changamoto kwenye baadhi ya maeneo. Tulikabidhi baadhi karibia maeneo saba, umeshatutatulia maeneo mawili, lakini bado yapo maeneo ya Kata za Isamilo, kuna kiwanja Na. 359 Block D ambayo ni ya Mtaa wa Isamilo Kaskazini A, Kaskazini B pamoja na Neshen.

Mheshimiwa NaibuSpika, pia kipo kiwanja Na. 590 cha Block C kule Nyegezi kati ya Mtaa wa Ibanda, Swila, Igubinya pamoja na Punzenza. Ninaamini maeneo haya yote Mheshimiwa Waziri akitumia utaratibu ule na ikiwezekana hata kwenye ile asilimia moja kama alivyofanya akaongeza asilimia ikawa mbili itasaidia lile deni liendelee kujifidia kule na wananchi wapate uhalali wa kuishi kwenye lile eneo kama walivyojenga na hatimaye waweze kulipa kodi ili tuweze kuondokana na kelele ambazo hazina shida sana.

Mheshimiwa Naibu Spika na Mheshimiwa Waziri, ninaamini kazi hii ambayo umeianza kwa muda mrefu na sasa tukiwa kwenye Awamu ya Sita, sina shaka tutakapofika 2025 kwa timu uliyonayo, wananchi wetu kwenye majiji haya; tunafahamu, ni kweli kwamba zoezi la upimaji na upangaji mara nyingi sana linaangalia maeneo ambayo bado hayajachangamka sana, lakini ukweli ni kwamba, maeneo yaliyochangamka sana kama Jiji la Mwanza la Mbeya na maeneo mengine, yanahitaji sana zoezi hili ili yaweze kuwa bora zaidi na Serikali na Wizara yako pia iweze kuingiza fedha za kutosha kupitia kodi ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la mwisho kwa leo, napenda niizungumizie hii premium ambayo inalipwa kwenye masuala mazima ya upatikanaji wa ardhi. Ninafahamu miaka michache iliyopita tulikuwa na utaratibu mzuri sana, ilikuwa fedha hii inatumika kama revolving fund. Pale Halmashauri zinapotumia, zinapopima, kumilikisha na kupanga, zile gharama zote zinazopatikana, Wizara ilikuwa na utaratibu wa kurejesha asilimia 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu baadaye mambo yakabadilika fedha hizi zikawa hazirudi, lakini sasa hii Mheshimiwa Waziri naomba niilete kwako kama ombi, Halmashauri hizi ambazo tunazitegemea zilipe fidia kwenye maeneo ya masoko, shule, hospitali, kwenye maeneo mbalimbali ya viwanja na kadhalika, zinakuwa na mzigo mkubwa. Unaweza kukuta Halmashauri kama ya ndugu yangu Mheshimiwa Deo hapa labda inaingiza shilingi bilioni mbili au tatu, atawezaje kulipa fidia? Atawezaje kulipa mapato mbalimbali ili aweze kukamilisha mahitaji haya? Kwa hiyo, mliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, uzuri Mheshimiwa Waziri anao mpango, aidha aendelee kuturudishia hii asilimia 30 au aendelee kutukopesha ile mikopo ambayo ametukopesha kwa muda mrefu na mifano mizuri ya matumizi bora ya hii fedha yapo. Ukiangalia leo Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, jirani pale kwa Mheshimiwa Mama Angelina Mabula, Mbunge na Naibu Waziri, aliwakopesha karibia shilingi 1,500,000,000/=, wamefanya vizuri hakuna mfano na ninawapongeza sana. Kwa sababu wameweza kurejesha fedha, yote na kupitia fedha hiyo wamepima na wamepata faida. Wamepima kwenya kata nyingi; kwa mfano, wamepima Kata ya Kirumba, Kata ya Shibura, Kata ya Buswelu, Sangabuye na hata Nyamongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Waziri, fedha hizi hebu tuletee. Hata Mwanza Jiji tunazihitaji.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo wa Spika.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mwongozo wa Spika.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Mbeya watakuwa wanazihitaji.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mwongozo wa Spika.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, tukipata fedha hizi za kutosha, sina shaka tutazitumia vizuri na tutarejesha kama walivyofanya Ilemela. Huu naomba uwe mfano wa kuigwa kwa sababu faida iliyopatikana na kazi iliyofanyika, leo hata wakiomba tena Mheshimiwa Waziri, wape zaidi ya shilingi bilioni 1.5 uliyowapa kwa sababu wameonyesha mfano. Nasi Jiji la Mwanza tumeomba kama shilingi bilioni tatu tu, tupe hizi fedha ili tufanya kazi hiyo na tuweze kupima na kupanga vizuri mji wako ili wananchi wako ikifika 2025 kura zote ziende kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sina shaka na Mheshimiwa Waziri, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, Mungu aendelee kuwabariki Wizara hii kazi nzuri.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. STANSLAUS S. MABULA – MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, na mimi nitumie nafasi hii kwanza kukushukuru sana kwa uamuzi wako uliopelekea Bunge lako kuifanya kazi hii kwa siku takribani nne ambazo hakika Wabunge wameisaidia sana Seriakli kuonesha namna ambavyo usimamizi, changamoto na mapungufu yaliyopo katika utendaji wa halmashauri zetu nchini. Ni mategemeo yetu kwamba mambo mengi yatazingatiwa leo baada tu ya maazimio haya ili yakaweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kabla sijaenda kwenye maazimio ya Bunge lako, yako mambo mawili ambayo nilitamani niyaseme. Moja ni lile la asilimia 10 ambalo Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamelizungumza, na wamelizungumza kwa sababu wanaamini kwamba fedha hizi ni nyingi sana; zingeweza kulisaidia sana Taifa kama malengo yake yalivyo.

Mheshimiwa Spika, msingi mmoja ambao umetushangaza sana Kamati, kwa sababu, ipo Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa, katika Sura 209 imeeleza wazi, na bahati nzuri sana imeitaja Kamati ya Huduma za Mikopo. Kamati hii kwenye kanuni ya 14 (1) inaundwa na Mkurugenzi mwenyewe wa Halmashauri, Muweka hazina wa halmashauri, Afisa Mipango, Afisa Ushirika, Afisa Ustawi na Afisa Maendeleo. Maana yake ni nini? Watu wote hao ni Wakuu wa Idara wenye weledi na wenye sifa za kusimamia kazi hii. Kwa hiyo tulitegemea sana kuona kwamba tunapozungumzia mapungufu kwenye eneo la asilimia kumi ambayo tunatarajia iende kwenye jamii na ikalete matokeo chanya haifanyi kazi yake sawa sawa. Tafsiri yake ni kwamba, inawezekana tuna watu ambao hawana uwezo wa kusimamia majukumu waliopewa.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo lilitutafakarisha sana ni suala la matumizi ya POS. Hizi POS zililetwa ili zisaidie, na mfumo huu umeletwa ili uisaidie Serikali katika ukusanyaji wa mapato na uirahisishie, lakini kumekuwa na mchezo ambao unaendelea kwenye matumizi ya POS, unakuta POS imezimwa kati ya siku 1000 mpaka 4,000. Maana yake ni kwamba, ikizimwa POS kwa siku 4,000 unazungumzia miaka zaidi ya mitatu mbele. Nyingine imezimwa zaidi ya siku 1,000 nyuma. Yaani hata kabla ya mfumo wa POS haujaanzishwa, POS imeshakuwepo na imezimwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tafsiri yake ni kwamba watu wanazima mashine na kurudisha mfumo nyuma wakati hela inayokusanywa haitoonekana popote pale. Na ile iliyopelekwa mbele maana yake ni kwamba ile fedha hautaiona wewe ambaye ni msimamizi pale. Kwa hiyo tunadhani yapo majukumu na ulazima kabisa wa Serikali kusimamia hili jambo na kuweka mifumo ambayo itatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kabla sijasoma maazimio ya Bunge lako, nijielekeze kwenye maelezo mafupi sana ya utangulizi. Kifungu cha 10 cha Sheria ya Ukaguzi wa Umma ya Mwaka 2008 kinatamka bayana kwamba ukaguzi unaotekelezwa na CAG ni kwa niaba ya Bunge. Naomba kuliarifu Bunge lako kwamba LAAC imejiridhisha kwamba kuwa ukaguzi wa hesabu za mwaka wa fedha ulioishia tarehe 30 Juni 2021 ulizingatia misingi ya Katiba na Sheria za nchi na viwango vya Kimataifa na Kitaifa. Katika kufikia hoja za ukaguzi zilizojadiliwa na Kamati. Aidha, kifungu cha 16 cha nyongeza ya nane ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Juni 2020 kimeweka Sharti la kwamba msingi wa kazi za LAAC ni taarifa ya ukaguzi uliotekelezwa na CAG.

Mheshimiwa Spika, Kwa sababu hizo, mapendekezo ya maazimio ambayo nitayawasilisha hivi punde yanatokana na uchambuzi wa Kamati kuhusi ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali wa Hesabu za Serikali kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa mwaka wa Fedha ulioishia Juni 2021. Aidha, maazimio haya pia yamezingatia michango ya Waheshimiwa Wabunge mbali mbali ambayo imetolewa hapa Bungeni kwa kujadili taarifa hii ya Kamati.

Mheshimiwa Spika, Wabunge zaidi ya 82, miongoni mwao Wabunge 71 wamechangia juu ya taarifa ya Kamati ya LAAC, na uchangiaji wao umetusaidia sana kuboresha maazimio yetu tuliokuwa tumeyatengeneza na kuyatoa awali. Ni matumaini ya Kamati ya kwamba maazimio haya yatasaidia katika kuimarisha usimamizi wa matumizi ya fedha za umma katika kuimarisha uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba uniruhusu nijielekeze kuwasilisha mapendekezo, hasa nijielekeze kuwasilisha maazimio kumi na moja kama ifuatavyo: -

(1) Mheshimiwa Spika, azimio la kwanza ni kuhusu mfuko wa mikopo kwa vikundi vya kina mama, vijana na wenye ulemavu. Ukaguzi uliofanywa na CAG umeonyesha kasoro mbalimbali za uendeshaji wa mfuko huu ikiwemo: -

(a) Halmashauri 155 kushindwa kukusanya shilingi bilioni 47.01 zilizotolewa kwa vikundi mbali mbali.

(b) Halmashauri 11 kushindwa kuhamisha shilingi bilioni 1.24 kutoka Akaunti ya Amana kwenda akaunti ya mifuko.

(c) Halmashauri 17 zilitoa mikopo ya shilingi bilioni 3.26 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu bila kuzungatia uwiano ulioanishwa.

(d) Halmashauri 83 kutokuchangia jumla ya shilingi bilioni 6.68 kwenye mfuko kutoka kwenye mapatao yake ya ndani.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Bunge linaazimia ya kwamba, Mamlaka ya nidhamu ya Wakurugenzi ichukue hatua dhidi ya Wakurugenzi wote waliobanika kushindwa kwa uzembe kusimamia kikamilifu utoaji na usimamizi wa mikopo hii kama ilivyoelekezwa kwenye kanuni ya 24(2) ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. (Makofi)

(2) Mheshimiwa Spika, kuhusu upatikanaji wa ruzuku ya maendeleo katika mamlaka za Serikali za Mitaa. Bunge linaitaka Serikali kutekeleza yatuatayo: -

(a) Kuzingatia matakwa ya sharia ya matumizi ya fedha zinazopitishwa na Bunge katika kila Mwaka wa Bajeti ili kuendelea kujijengea imani Bungeni na kwa wananchi.

(b) Kuweka angalau karibio kwa kiasi cha ruzuku endapo itabidi baadhi ya halmashauri kuzidishiwa kuliko vile inavyotokea kwamba halmashauri zingine hupewa kiasi kidogo mno wakati zingine hupewa zaidi ya asilimia hamsini.

(c) Kutorejesha Hazina fedha zinazokuwa zimepelekwa katika halmashauri kwa madai kuwa mwaka husika wa fedha umeisha ili kukamilisha miradi inayohusika.

(3) Mheshimiwa Spika, kuhusu uwekezaji wa tija, kuhusu uwekevu na tija katika uwekezaji wa mitaji ya umma. Ukaguzi umebainisha dosari zinazohusu uwekezaji wa mitaji ya umma katika baadhi ya halmashauri nchini.

Mheshimiwa Spika, dosari hizo ni pamoja na uwekezaji unaofanyika bila upembuzi yakinifu wala andiko la biashara. Bunge linaitaka Serikali, kuhakikisha kuwa halmashauri zote zinazofanya uwekezaji, unazingatia fursa za uwekezaji na tija katika maeneo mbalimbali ya halmashauri kuliko hali ilivyo sasa ambapo kila halmashauri inataka kuwekeza kwenye soko na kituo cha mabasi tu. Aidha, Serikali iandae muongozo na kanuni inayoelekeza namna bora ya uwekezaji kwa ngazi za halmashauri na kuzingatia umuhimu wa maandiko miradi kabla ya kuanza miradi husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nne, kuhusu manunuzi na mikataba ya upatikanaji wa huduma na bidhaa. Ukaguzi umebaini udhaifu katika ununuzi na upatikanaji wa huduma na bidhaa katika halmashauri bila kufuata taratibu zinazohusika. Hali hiyo inaweka mwanya wa upotevu wa fedha za Umma. Hivyo basi, Bunge linaiagiza Serikali kusimamia ipasavyo manunuzi yote ya Umma kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa na kwa kuridhiwa na Bunge. Aidha, Maafisa Masuuli wote watakaobainika kutosimamia ipasavyo agizo hili, wachukuliwe hatua kali za kisheria kwa nia ya kukomesha ubadhirifu na kuliletea Taifa manufaa stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tano, kuhusu upatikanaji wa stahiki za watumishi kwa mujibu wa sheria. Bunge linaitaka Serikali kushughulikia mara moja madai yote ya stahiki za watumishi wa halmashauri kwa mujibu wa sheria ambazo hazijatolewa na kuchukua hatua kali kwa waajiri wasiozingatia matakwa ya sheria zinazohusika na stahili za watumishi.

Mheshimiwa Spika, sita, kuhusu ukusanyaji wa mapato ya ndani ya halmashauri. Imebainika kwamba halmashauri zilizo nyingi zina udhaifu katika eneo la ukusanyaji wa mapato ya ndani kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo upotevu wa mapato kwenye mifumo ya kielektroniki, rushwa na kutosimamia ipasavyo sheria, kanuni na taratibu za kifedha; hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kutekeleza yafuatayo: -

(a) Kuhakikisha kuwa mfumo mpya wa ukusanyaji wa mapato, yaani TAUSI, unaanza kutumika katika halmashauri zote za Serikali nchini ndani ya mwaka wa fedha wa 2022/2023;

(b) Kuchukua hatua kali za kisheria kwa watendaji wote ambao wanakusanya mapato nje ya utaratibu wa kisheria na ambao hawapeleki makusanyo hayo benki kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, saba, kuhusu matumizi yasiyofaa ya fedha katika Akaunti za Amana. Imebainika ya kwamba katika halmashauri mbalimbali fedha zilizomo katika Akaunti za Amana zinatumika kwa shughuli ambazo hazikutarajiwa. Ripoti ya CAG ilibainisha matumizi mabaya ya Shilingi bilioni 9.74 kutoka katika Akaunti za Amana kutokana na kutosimamiwa ipasavyo. Matumizi hayo yalibainika katika halmashauri 81 nchini na hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kuhakikisha kuwa fedha zinazowekwa katika Akaunti za Amana zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa kuliko hali ilivyo sasa ambapo akaunti hizo zinaonekana kutumika kama maficho ya fedha ambazo baadaye hutumika kibadhirifu.

Mheshimiwa Spika, aidha, Maafisa Masuuli wote waliotumia fedha hizi kinyume na uataratibu wachukuliwe hatua kali za kinidhamu. Mifano ipo kama ambavyo tuliitaja, kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa ilitumia zaidi ya Shilingi milioni 90 bila utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, azimio la nane, kuhusu upotevu wa mapato katika mifumo ya kielektroniki ya kukusanyia mapato. Imebainika kuwepo kwa upotevu wa mapato kupitia katika mifumo ya kielektroniki katika halmashauri zetu. Katika mwaka wa fedha 2021, halmashauri 27 zilifanya marekebisho ya miamala yenye jumla ya Shilingi bilioni 1.6 kwenye mfumo bila uthibitisho wa ulazima na uhalali wa marekebisho hayo kufanyika. Hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kuchukua hatua kali za kinidhamu kwa watumishi wote waliohusika na upotevu, mathalan watumishi walio katika halmashauri ambazo miamala ya mapato ilibadilishwa au kufutwa bila uthibitisho wa ulazima wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tisa, kuhusu hasara ya kifedha kutokana na vitendo vya taasisi za Serikali dhidi ya halmashauri. Imebainika kuwa, jumla ya Shilingi bilioni 2.34 hazijalipwa katika mamlaka mbalimbali za Serikali za Mitaa nchini kutokana na huduma za tiba zilizotolewa kwa wanufaika wa mfuko huo. Hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kushughulikia mara moja suala la NHIF kutorejesha gharama za matibabu na vifaatiba vinavyotolewa na halmashauri kwa wanufaika wa bima ya afya chini ya mfuko huo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini.

Mheshimiwa Spika, Bohari ya Madawa (MSD); Halmashauri nyingi zimekuwa zikilipa fedha kwa bohari ya madawa nchini (MSD) pasipo kupelekewa dawa na vifaatiba kwa wakati. Zaidi ya Shilingi bilioni 1.17 hazijawahi kupelekwa kwenye vituo dawa za gharama hiyo. Hivyo Bunge linaitaka Serikali kuisimamia ipasavyo MSD ili iwe inapeleka dawa na vifaatiba katika halmashauri kwa muda usiozidi mwezi mmoja kulingana na mahitaji ya halmashauri husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Huduma za Ununuzi Serikalini (GPSA). Imebainika kuwa halmashauri mbalimbali zimekuwa zikiamrishwa au zikihimizwa kupeleka fedha kabla ya kupata huduma au bidhaa husika kwa upande wa uagizaji na manunuzi ya magari. Wameshindwa kufanya vizuri kwani wamekuwa na tabia ya kurudisha fedha kwa wateja pasipo kukamilisha manunuzi ya magari hayo kwa muda uliopangwa. Hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kuisimamia GPSA ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa weledi na kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi zao ili kuzisaidia halmashauri katika utekelezaji wa mipango yao kuliko hali ilivyo sasa ambapo GPSA huchangia kuzizorotesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA). Bunge linaitaka Serikali kuimarisha TEMESA ili iweze kuzisaidia halmashauri na taasisi nyingine za Serikali ili kupunguza malalamiko ya udhaifu wake katika eneo la ukaguzi na utengenezaji wa magari na mitambo katika halmashauri.

Mheshimiwa Spika, azimio la kumi, kuhusu uteketezaji wa dawa za binadamu katika halmashauri na vituo vya afya. Taarifa ya CAG ya mwaka wa fedha 2021 inaonesha kuwepo kwa wimbi kubwa la uteketezaji wa dawa za binadamu zenye thamani kubwa ya fedha. Kwa miaka mitatu tuliyotolea mfano, zaidi ya Shilingi bilioni 12.3 katika halmashauri 91 dawa zake ziliteketezwa. Hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa hazipokei dawa zilizobakiza muda wa matumizi unaopungua miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, azimio la 11, upungufu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Uchambuzi wa Kamati kutokana na taarifa ya CAG umebainisha kuwa, baadhi ya halmashauri hazina watumishi wenye taaluma unaohitajika na kulazimika kutumia watumishi wasio na sifa kwa kazi zinazohitaji utaalamu. Kitendo hiki kinasababisha kufanyika kwa maamuzi yanayosababisha hasara kubwa katika halmashauri zetu. Hivyo basi, Bunge linaitaka Serikali kupeleka katika kila halmashauri wataalamu wa kutosha kwenye sekta zote muhimu zinazohitajika katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuwatumia ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kukushukuru wewe na Waheshimiwa Wabunge wote kwa mijadala mizuri.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na inawezekana nikawa msemaji wa mwisho kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze tu kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri na za msingi ambazo anaendelea kuzifanya. Lakini natakata tu niwakumbushe ndugu zangu tulioko humu ndani na ndugu zangu Wabunge wa CCM wala msipate shida msishangae. Ni ajabu sana leo tunazungumza masuala ya bajeti ya kuwasaidia Watanzania watu bado tunawaza uchaguzi wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana baada ya uchaguzi 2015 Wananchi waliamua kutenganisha. Kuongoza nchi si sawasawa na kuongoza SACCOS. Wananchi wa Tanzania walipoamau kuichagua CCM waliamini Mheshimiwa Magufuli atakwenda kuongoza Serikali. Serikali tunayoizungumza ni Serikali yenye mifumo inayoweka utaratibu wa kuwasaidia wananchi wanyonge maskini na wahali ya katikati. Sasa leo ndiyo maana yako makundi haya, uwezo wa kuongoza SACCOS na uwezo wa kuendesha nchi ni vitu viwili tofauti. Tunachangia bajeti mwaka 2017/2018 naomba niwakumbushe tunapokwenda kwenye utaratibu wa ukusanyaji wa kodi, ziko kodi ambazo zimeandikwa kwenye schedule ya leseni ziko biashara ambazo hazijatambulika. Biashara hizi zinazifanya Halmashauri zinazokusanya kodi ziwe na tabia tofauti tofauti. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, mnapokwenda kwenye kipengele hiki tuangalie ili kuweka uwiano ambao utakuwa unafanana karibu kwenye Halmashauri zote nchini. Lakini nikumbushe hapa, nimshukuru tena Waziri pamoja na Mheshimiwa Rais na sisi Wabunge sote wa CCM ambao tulikaa hapa kupanga kuhakikisha wafanyabiashara ndogo ndogo wanatambuliwa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo rafiki yangu Comrade Mwakajoka amenishangaza sana, anataka kuwatisha umma wa wafanyabiashara ndogo ndogo nchi kwamba wataanza kulipa kodi, kodi ambayo ukikisoma kitabu hiki hakuna popote ilipoandikwa Mmachinga, mama lishe, mama ntilie, anayeuza mitumba, anayeuza hiki kwamba anakwenda kutambulika na kulipa kodi. Wakati tunasimama hapa tunawapigania wanyonge hawa na mimi najua ndugu yangu Mwakajoka hili kwenu ni pengo upande mwingine hili ni pengo, kwa sababu hawa wafanyabiashara ndogo ndogo ndiyo walikuwa wanatumika isivyo kuhakikisha wanakuwa mbele kusaidia watu kupita mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amezunguka nchi nzima ameona machinga wanavyopata taabu, kaona mama lishe wanavyopata taabu, leo amewatambua na wao watambulike na wao wawe rasmi waache kufukuzwa na mabomu, waache kupigwa, waache kunyanyasika leo tunasema wanatengenezewa kodi ili waanze kuogopa mapema. Ni lazima tuwe na shukrani kwenye mambo yasiyokuwa yanafaa, na mimi nilitegea sana kaka yangu Sugu hata Waitara wangekuwa wakwanza kupongeza kwenye utambuzi wa wafanyabiashara ndogo ndogo maana wao ndio wanaathirika pale sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda ni mfupi lakini nizungumze suala la kodi ya majengo. Wakati Serikali ilipoingilia suala la kukusanya kodi za majengo mwaka wa jana; zilipoondolewa kwenye Halmashauri haraka haraka wote tulifikiria kwamba Serikali imekosea. Nataka niwaambie, Mheshimiwa Rais alitazama mbali na akafikiria jambo la mfano mzuri sana.

Leo tunawaza habari ya vyanzo vipya vya mapato, ninyi nyote ni mashahidi nyumba ambazo zilikuwa hajafanyiwa evaluation zilikuwa hazilipi kodi ya pango zilikuwa hazilipi kodi hii muda mrefu. Leo pigia hesabu nyumba ngapi ambazo hazijafanyiwa evaluation katika nchi hii zitalipa kodi? Na leo zinakwenda kulipa kodi ambayo itakuwa inakwenda kusaidia kwenye nyanja mbalimbali tunazosema kuongeza dawa, barabara lakini kuimarisha vituo vyetu vya afya na kadha wa kadha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana ilikuwa ni lazima hii kupigiwa kelele, Halmashauri zimetumia vibaya sana fedha hizi na mfano mzuri ni Arusha. Arusha imekuwa Jiji ililokuwa na tofauti Diwani akienda kwenye kikao kimoja analipwa zaidi ya shilingi 800,000; lakini ukienda Mwanza na maeneo mengine anambuliwa shilingi 200,000 iliyoko kwenye utaratibu. Ni lazima tusimame kuikusanya fedha ya Serikali ikawasaidie wananchi walio wanyonge. Kwa nini tusiipongeze Serikali? Sote tunafahamu na mimi niwakumbushe huwezi kuwa ndani ya nyumba hii kikiamuliwa kitu wewe ukasimama pembeni, wewe ni sehemu ya maamuzi yote yanayofanyika kwenye nyumba hii na Watanzania wanalijua hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tukubali. Tunafahamu, kodi ya mabango pia imekwenda Serikalini na mimi niwashukuru Mheshimiwa Mpango naamini mmetengeneza utaratibu sahihi ambao fedha hii mtakapoikusanya kwa pamoja itakuwa inarudi kwenye Kata kwa wakati, kwenye Halmashauri zetu, kwenye Miji, Majiji na Manispaa ili iweze kufanya kazi yake sawa sawa. Tunafahamu jukumu la kupeleka asilimia tano kwa wanawake na vijana ni la Serikali ambao iko chini ya Chama cha Mapinduzi na hii iko kwenye Ilani tutatekeleza. Limejadiliwa suala la milioni hamsini hapa; wenye Ilani Chama cha Mapinduzi milioni 50 tumeahidi ndani ya miaka tano kwa nini mnataka tupeleke leo? Mimi ninayoimani kwamba fedha hizi zitakwenda, na zinatengenezewa utaratibu ili tuweze kufikia malengo tuliyokusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena, suala la kuongoza nchi lina tofauti kubwa sana na kuongoza kitu kingine cha kawaida ili kufikia malengo ya Watanzania. Mungu awabariki sana, ahsanteni kwa kunisikiliza. Naunga mkono hoja asilimia 100.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii na nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mungu lakini kukupongeza pia kwa kupata nafasi ya kuaminiwa na Bunge kwa ajili ya kutuongoza sisi wenzako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo napenda kuzungumzia mambo machache yasiyozidi matatu. Ningependa nianze na suala la kwanza ambalo kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu liko jambo ambalo amelizungumza katika ukurasa wa 37 linalohusu masuala ya Maliasili na Utalii pamoja na ukurasa wa 46 linalohusu viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu namna bora ya kusaidia utalii katika nchi hii ni pamoja na kuunga jitihada kubwa zilizofanywa na Mheshimiwa Rais katika Filamu yake ya Royal Tour ambayo imetusaidia sana kuleta watalii wengi nchini. Tumekuwa tukisema kila mara juu ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Natamani sana kuona bajeti hii tutakapokuwa tunakwenda kuihitimisha Uwanja wa Ndege wa Mwanza uwe umetengewa fedha zitakazokwenda kuujenga na kuukamilisha kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo sababu nyingi za kwa nini tunahitaji uwanja wa ndege wa Mwanza ukamilike. Hivi tunavyozungumza jana kule Arusha ndege ya KLM imeshindwa kutua kwa sababu za hitilafu ya uwanja na kulazimika watalii kwenda kushushwa Entebbe. Mpaka hivi ninavyozungumza inawezekana watalii wote waliokuwa wanakuja Tanzania kwa Ndege ya Shirika la KLM wako Entebbe na hawana namna tena ya kurudi hapa mpaka pale Wizara ya Maliasili na Utalii itakapojipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yangu ni nini? Laiti uwanja uliopo Mwanza ungekuwa umekamilika na kuwa Uwanja wa Kimataifa wa Ndege ingekuwa ni rahisi sana kwa ndege ya KLM kutua Mwanza na abiria wote wakaendelea na shughuli za utalii hapa hapa nchini. Kwa hiyo nitoe wito kwa Serikali kwamba jambo hili ni la muhimu na tulitazame upya kuhakikisha kwamba Mwanza ambayo tunaitazama kama hub ya utalii kwa kanda ya ziwa, basi iweze kufanikiwa na kutoa matunda ambayo tunayategemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nilitamani sana nizungumzie habari ya wafanyabiashara ndogo ndogo, Machinga. Niiombe sana Serikali, nafahamu imekuwa na utaratibu mzuri toka Mheshimiwa Rais alipotoa maelekezo wafanyabiashara ndogo ndogo nchini wote walitii na kwenda kwenye maeneo yaliyopangwa. Bahati mbaya sana ni maeneo machache sana yaliyojengwa kwa nguvu ya Serikali, maeneo mengi yamejengwa kwa nguvu za wananchi, wale wafanyabiashara wenyewe, lakini wajibu wa Serikali ilikuwa ni kuimarisha maeneo haya ya kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe sana Serikali, wafanyabiashara na Serikali itazame, yako mambo hakuna sababu ya kuyaunganisha nchi nzima. Ukizungumza habari ya wafanyabiashara ndogondogo nchi hii iko miji ukiitazama tu unaweza ukaichukua hiyo na ukatengeneza mazingira bora yatakayowasaidia wafanyabiashara, Mkoa wa Mwanza, Mkoa wa Dar es Salaam kwa ujumla wake, Mkoa wa Arusha, Mkoa wa Mbeya lakini na hii sio Mkoa kwa ujumla nikisema Mwanza namaanisha Manispaa ya Ilemela na Jiji la Mwanza per se.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamejenga masoko, lakini mpaka leo masoko hayana namna bora ya kuwasaidia hao wafanyabiashara. Tafsiri yake tunaanza kuwaacha holela na wanaanza kufikiria kurudi kule walikokuwa kwa sababu na wao kule waliko wanatafuta riziki na huwezi kuipata riziki kwenye mazingira magumu. Kwa hiyo nitumie nafasi hii kuiomba Serikali, pale Mwanza walitengewa maeneo ya Igoma kule kwa Ukwaju, wakatengewa Dampo kule maeneo ya Buhongwa, lakini wakatengewa eneo moja pale Mjini Igogo ambalo linaitwa eneo la Mchafukoga. Maeneo haya toka wamejenga wenyewe Serikali ikawekeza nguvu kidogo na sasa tulipopata milioni 500 na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kuipeleka pale Mchafukoga, fedha hii ni kidogo.

Kwa hiyo, niombe Serikali itazame upya, kama tumeamua kuwapanga wafanyabiashara na wamekubali kwenda kwenye maeneo tuliyowapanga, basi ni lazima tuchukue makusudi ya lazima kuhakikisha tunapeleka fedha kwenda kuboresha maeneo waliyopo ili waweze kufanya biashara zao kwa uhuru na wale wanaokwenda kununua wawe na amani ya kwenda kununua kwenye yale masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba masoko yote yako kiholela. Masoko yote hayana ubora wa kumfanya mtu atamani kwenda kununua kwenye yale masoko. Kwa hiyo kwa namna yoyote ile bado tunaendelea kuweka ukinzani kati ya wafanyabiashara na Serikali na tunafahamu halmashauri zetu. Ukichukulia mapato wanayokusanya, ukachukulia fedha inayokwenda kwenye miradi ya maendeleo, hata iweje ukiwaambia wawekeze fedha zingine kwenye kuboresha yale masoko bado haitawezekana na itaendelea kulaumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko hatua ambazo Mheshimiwa Rais alizielekeza na hatua hizi ni mahsusi. Niombe sana tunaposema Mheshimiwa Rais alielekeza maeneo yote waliyopangwa wafanyabiashara, usafiri wa daladala na mwingine utengenezewe mazingira ya kufika pale. Sasa inafika wakati Mbunge unashauri, Mkuu wa Wilaya anashauri, viongozi wengine wanashauri, lakini hakuna utekelezaji, maana yake ni nini? Hawa wafanyabiashara itafika wakati watachoka kwa sababu yale tuliyokubaliana nao hayatekelezeki na kufanya ugumu wa wanunuzi kushuka kwenye yale maeneo na kwenda kununua bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana, kwanza zichukuliwe hatua za dharula kuhakikisha maeneo yote tuliyotenga vinajengwa vituo vya daladala kwa lazima na kwa muda mfupi ili kuwarahisishia wanunuzi wafike kwenye maeneo hayo.

Pili, Serikali iwe na uwiano wa kupeleka fedha. Jiji la Mwanza ndio Jiji linaloongoza kwa wafanyabiashara wengi hapa nchini. Tuna wafanyabiashara, machinga, mama lishe na watu wa aina hiyo zaidi ya 12,000. Sasa ukichukua soko na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, tunajenga soko kubwa lakini uwezo wa soko hili utachukua watu takribani 1,400. Kati ya 1,400 ni machinga 200 peke yake ndio wanaweza kukaa humu ndani, lakini Ukwaju kuna Machinga zaidi ya 2,800, ukienda Buhongwa pale kuna Machinga zaidi ya 3,600, ukienda Mchafukoga kuna Machinga zaidi 2,000, lakini mazingira sio wezeshi kuwafanya watu wafike kwenye haya maeneo. Kwa hiyo, niombe sana kama tuna dhamira njema ile ambayo Mheshimiwa Rais ameikusudia na sisi wasaidizi wake tuwekeze nguvu kuhakikisha mazingira haya yanakuwa bora na yanafanyiwa kazi kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaomba sana kama tunayo dhamira njema, ile dhamira ambayo Mheshimiwa Rais ameikusudia, nasi wasaidizi wake tuwekeze nguvu kuhakikisha mazingira haya yanakuwa bora na yanafanyiwa kazi kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni kuhusu TASAF; katika jambo amblao nataka kuishukuru Serikali na kuishauri iendelee kuwekeza nguvu nyingi zaidi ni kwenye mpango mpya wa TASAF ambao unawekeza katika miundombinu ya kudumu kwenye sekta ya afya, sekta ya elimu na sekta ya barabara. Kwa kufanya hivi utakubaliana nami, fedha nyingi ambazo tumeshazitoa kwa watu zaidi ya 14,000 tukitafuta uhalisia na thamani yake leo hatutaupata kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Jenista Mhagama na hata ambapo amemuachia Mheshimiwa Simbachawene leo naamini kazi hii itaendelea. Ukienda pale Nyamagana peke yake tumepata ujenzi wa shule mpya pia tumepata ujenzi wa kituo kipya cha afya. Tumejenga barabara zaidi ya kilometa 416. Huu ni mpango ambao kupitia mradi wake wa OPEC, kama utaendelea hivi utawakwamua sana wananchi kwa ujumla wao wengi kuliko ilivyo hivi sasa inavyokwenda kwa mtu mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nyongeza ninaomba sana awamu ya pili ya OPEC ilitakiwa ianze mwezi huu wa Nne. Mradi huu unataka kusisitiza na nirudie kusema tena

Mheshimiwa Waziri Jenista ulipopita ziara yako wananchi wa Nyamagana wanakushukuru sana, hata leo umemuachia Kaka yako Simbachawene naamini na yeye atakuja kuhakikisha hii awamu ya pili ya mradi wa OPEC ambao tunategemea tupate Shule ya Sekondari kule Kata ya Igoma, tunategemea tujenge barabara nyingine kule ya Mabatini - Kleruu na tunategemea tupate mradi mwingine kwenye eneo lingine…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mabula.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa hiyo nachotaka kusema naunga mkono mapendekezo ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini tusisitize kupeleka fedha kwenye miradi unganishi ili iweze kuwasaidia wananchi. Nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia angalau kwa mambo machache ambayo nimeyapitia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kusimama mbele ya Bunge leo kuchangia nikiwa kama mmoja wa Wajumbe wa Kamati zilizowasilisha ripoti zake leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na namna ambavyo CAG ametuonesha matumizi mabaya ya Ofisi ya ALAT. Ni ukweli usiopingika kwamba chombo cha ALAT kinachounganishwa na Halmashauri zote nchini, kinapokusanya fedha zake kinakusanya fedha kwa lengo la kuendesha chombo hiki na kila Halmashauri nchini inachanga fedha kwa ajili ya chombo hiki kuendeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka michache iliyopita ALAT ilikusudia kujenga jengo kwenye Mji wa Dodoma lakini kama CAG alivyotuonesha, kwenye milioni 523 kati ya fedha hizo milioni 367 hazionekani wapi zimekwenda. Kamati ya PAC imeliona hili na kulileta kwenye Bunge lako ili Bunge lako liweze kushauri vinginevyo lakini kuchukua hatua stahiki juu ya fedha za wananchi kutoka kwenye Halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende haraka haraka kidogo kwa sababu najua muda wangu ni mchache. Lipo suala la urejeshaji wa fedha kutoka TRA kwenda kwenye taasisi mbalimbali za Serikali, tulitamani sana kama ambavyo makubaliano na mujibu unavyotaka fedha zote zinazokusanywa kutoka Halmashauri, kutoka wapi, inapofika wakati kwa mujibu wa sheria na misingi ile ya kuendana na bajeti zilizopangwa, fedha hizi ziende kule kwenye halmashauri zikafanye kazi yake sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa kidogo, hawa Wakurugenzi wanaopigwa mawe hii tabia ya kuzungumza unaenda mbele unarudi nyuma, ndugu yangu, Mheshimiwa Heche amesahau kidogo, dakika chache zilizopita Mheshimiwa Gekul hapa ametupa mfano bora watu tukajifunze Babati kwamba pale kuna Mkurugenzi makini anayefanya kazi yake sawasawa. Sasa matatizo ya mtu mmoja hayawezi kujumlisha Wakurugenzi zaidi ya 168, ni lazima tukubali na twende na kauli hiyo, itatusaidia kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa PAC Mheshimiwa Heche amezungumza hapa habari za NIDA, habari za vitambulisho na kadhalika. Kamati ya PAC ilipokuwa inapitia taarifa zake mbalimbali, zipo taarifa zitakuja kwa wakati mahsusi na yapo mambo kama hayajakamilika hayana sababu ya kuja kwenye Bunge hili! Hii ni sambamba na taarifa ya mradi wa Dege, Kamati imeunda Kamati ndogo imetengeneza taarifa zake vizuri imepeleka kwa Spika zimeanza kufanyiwa kazi, Bunge tusubiri taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni lazima tukubali. Umezungumzwa hapa mradi wa Mlimani City, umetajwa mradi wenye maajabu saba, ni kweli. Mradi wa Mlimani City leo una takribani miaka 11, mradi huu toka uanzishwe tunataka kusema pamoja na changamoto zake ambazo CAG ameziona, kama Kamati tumezielewa. Siyo hili tu la mradi mbovu, tunaongelea habari ya Chuo Kikuu cha Mlimani kinachotoa wataalam waliobobea, kinachotoa ma- Profesa, leo ametajwa humu Waziri wa Sheria, Mheshimiwa Profesa Kabudi pale na wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo mimi niwaulize kwa makosa ya mtu mmoja kuingia mikataba mibovu, mnataka kusema watu wote waliopita Chuo Kikuu cha Mlimani uwezo wao ni dhaifu? Kwa sababu ni lazima tukubali changamoto hizi zipo na kama changamoto hizi zipo, kwa mfano, mradi huu toka ulipoanzishwa sote tunafahamu zipo faida kubwa zimeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulipojengwa mradi wa Mlimani City tunaamini eneo lile limeongezeka thamani, pamoja na matatizo ya Mlimani City sote tunafahamu miaka 11 iliyopita ukirudisha miaka minne nyuma, Chuo Kikuu cha Mlimani kimekuwa kikipata bilioni 16 na pointi kama gawio kutoka Chuo Kikuu, fedha hizi zinaiwezesha Mlimani City kujihudumia kwenye bajeti yake kwa asilimia 28. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifanya hesabu ya kawaida sote tunakubali Mlimani City ina matatizo ya kimkataba na waliohusika wapo na hatua zimeshaanza kuchukuliwa baada ya CAG kutoa ripoti hii. Tunachokisema sasa Serikali baada ya mradi huu tutulie twende polepole, tunaongea facts hapa, hatupigi kelele, tunaongea facts hapa! Serikali kila mwaka inapata kodi ya VAT… (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila mpangilio)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Serikali kila mwaka inapata kodi ya VAT bilioni 18 kutoka Mlimani City kwenye biashara zote zilizopo pale. Sote tunakubali property tax takribani milioni 150, lakini tax levy ya Manispaa ya Ubungo zaidi ya milioni 72. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosema, Kamati imebaini matatizo kwenye Mkataba wa Mlimani City. Tunaiomba Serikali iangalie na ifanye kazi vizuri kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naomba Bunge lako liweze kuunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nitumie fursa hii kukushukuru na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu kwa ajili ya maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kwamba kazi kubwa inayofanywa na sekta hii au Wizara hii ya Afya inasaidia sana katika kuhakikisha Watanzania wanaendelea kuwa na afya bora, lakini watoto ambao wanazaliwa na wenyewe pia wanazaliwa kwenye mazingira mazuri yanayowafanya na wao wawe watu ambao mwisho wa siku watakuwa sehemu ya watu wa kutegemewa kwenye Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze mambo manne peke yake. Kwanza nizungumze juu ya upatikanaji wa madawa. Sote tunafahamu Serikali imefanya jitihada kubwa sana hasa katika suala zima la upatikanaji wa dawa. Taarifa iliyosomwa hapa na Mheshimiwa Waziri pia na Kamati inaonesha tumekwenda karibu asilimia 89 kwa mwaka 2017/2018, hii ni hatua moja kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, bado liko tatizo kule kwenye jamii. Watu wengi sana hawaelewi hizi dawa muhimu tunazozizungumza ni zipi, lakini dawa ambayo inapatikana kwenye zahanati, dawa ambayo inapatikana hospitali ya Wilaya unaweza usiipate kwenye kituo cha afya au kwenye zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe Wizara ichukue jambo hili kama sehemu ya utatuzi na elimu kwa jamii, itengeneze utaratibu kuanzia ngazi ya zahanati, ieleweke mtu anayekwenda kwenye zahanati ziko dawa za aina gani atakazozipata, akiwa kituo cha afya atapata dawa ya aina gani na hospitali ya Wilaya atapata dawa ya aina gani, kwa sababu hili linatukumba hata sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwananchi anaweza kupiga simu yuko kwenye kituo cha afya anasema dawa hii hakuna, lakini ukweli ni kwamba dawa ile wakati ule pale alipo siyo sehemu yake. Sasa hii lazima tujitahidi sana kutoa elimu ya kutosha ili muweze kutusaidia tuepuke matatizo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu juhudi kubwa zinazofanya na Serikali bila kuangalia motisha au haki za watumishi kule waliko na wanazozitegemea na zingine siyo kubwa sana Mheshimiwa Waziri. Kwa mfano, nimwombe sana, zile allowance za uniform zinazopatikana kwa mwaka pia allowance za likizo zao, lakini pia on call allowance, haya ni mambo ambayo yatatusaidia kuboresha zaidi huduma zetu za kiafya hasa kwa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watumishi ni wengi sana lakini pamoja na kazi kubwa wanayoifanya Mheshimiwa Waziri tunaamini kabisa kwamba tukiwatazama na wao kwa jicho jingine kwamba ni sehemu yetu na kazi hii ni kazi ya wito. Kazi ya wito ukipata stahiki zako ambazo ziko kwa mujibu wa sheria na wewe utaifanya kwa malengo yale yale uliyojiwekea na utakuwa umepiga hatua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri, kwenye hotuba yake ameonesha moja ya kipaumbele ni kuhakikisha anaboresha miundombinu ya hospitali. Mheshimiwa Waziri hili ni jambo kubwa sana, miundombinu ya hospitali zetu nyingi kwa muda mrefu imekuwa siyo rafiki lakini kwa sasa amejitahidi sana kwa kufanya jambo hili. Hapa nazungumzia kuanzia kwenye ngazi ya zahanati, ngazi ya vituo vya afya lakini hospitali za Wilaya na hospitali za Rufaa za Mikoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwanza Jimbo langu la Nyamagana ndipo ilipo hospitali ya Rufaa ya Mkoa hospitali ya Sekou Toure, lakini ndipo ambapo nina hospitali ya Wilaya ya Nyamagana ambayo iko Butimba. Nikianza na hospitali yetu ya Sekou Toure, hospitali hii imekuwa ni hospitali tegemeo lakini imekuwa ni hospitali kubwa ya muda mrefu na nimshukuru sana ameiangalia kwa muda mfupi aliokuwepo hospitali yetu kwa sasa imekuwa bora sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hizi haziwezi zikaboreka bila kuangalia umuhimu wa watu ambao wamefanya kazi kwenye maeneo haya. Nitumie nafasi hii nimpongeze sana ndugu yangu na rafiki yangu Dkt. Leonard Subi ambaye amekuwa RMO pale, lakini nimpongeze Katibu wake Ndugu Temba. Niwapongeze na Waganga wafawidhi mama yangu Onesmo ambaye leo ni mstaafu lakini dada yangu Bahati Msaki ambaye sasa anashikilia nafasi ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuficha ni kwamba hospitali hizi pamoja na wataalam tulionao bila kutumia weledi wao na ubora na moyo wao wa dhati wa kujitoa mazingira ya hospitali haya hayawezi kubadilika. Leo ukienda hospitali ya Sekou Toure ni sawa unazungumza hospitali tofauti kabisa na ilivyokuwa miaka mitatu huko nyuma iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni pongezi kubwa kwa watumishi wote, lakini jitihada zinazofanywa na Serikali na utashi wa watu wenyewe waliopewa jukumu hili na nimeambia Dkt. Subi amepanda daraja kidogo. Nimpongeze sana kwa sababu jitihada alizozifanya Sekou Toure anastahili na sifa hiyo anastahili kwenda hapo alipo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maboresho makubwa haya ya hospitali ya Sekou Toure ambayo kwa kweli ni hospitali ya Kanda ya Kimkoa, tunaitegema kwa nguvu nyingi, nimwombe sana liko jambo moja pamoja na ubora huu hospitali hii haina CT Scan. Sote tunafahamu tukiongeza CT Scan kwa sasa, mapato yaliyoongezeka kutoka shilingi milioni 30 kwa mwezi mpaka milioni 120, leo ukiongeza CT Scan utakuwa umeiongezea uwezo mkubwa lakini kingine tuongeze Madaktari bingwa kushughulika matatizo ya kibingwa ili wawepo kwa wingi waweze kusaidia umma wa watu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba na jengo tunalolijenga sasa hivi kwenye hospitali ye Sekou Toure, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri tumepata bilioni moja kwa mwaka huu, imefanya kazi kubwa na Mkoa wa Mwanza ni moja kati ya mikoa nane ambayo kwa kweli imetajwa katika matatizo ya vifo vya mama na mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kukamilika kwa jengo hili kwa wakati itakuwa imetusaidia sana kuhakikisha kwamba vifo vya mama na mtoto ambao ni sehemu ya kipaumbele cha Mheshimiwa Waziri, atakuwa ametusaidia lakini atakuwa amesaidia akinamama wa Mkoa wa Mwanza na wale wa mikoa ya jirani kuja kupata huduma hizi kwa kiwango cha hali ya juu, tukiamini mpango huu wa malipo kwa ufanisi utakuwa na tija na utatoa matunda ambayo ni stahiki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze juu ya habari ya uboreshaji wa huduma za afya kwenye hospitali zetu za Wilaya. Tunayo hospitali yetu ya Wilaya ya Nyamagana. Hospitali hii ilianza miaka mingi ikiwa kama zahanati ikapandishwa daraja kuwa kituo cha afya na sasa ni hospitali ya Wilaya. Ukweli usiofichika nirudie tena kusema Watumishi hawa Madaktari, Wauguzi na Wakunga wanafanya kazi kubwa sana. Hospitali hii miaka miwili iliyopita kabla hatujawa na dawa za uhakika, kabla hatujawa na uhakika wa kukabiliana na kushughulika na matatizo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kupata muda angalau wa kuchangia nami niseme mambo machache ambayo nadhani yanaweza kutusaidia hasa tunapozungumza juu ya habari ya miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba Wizara hii haihusiki sana na TARURA, lakini fedha zinazotoka katika Mfuko wa Barabara ni sehemu ya fedha zinazokwenda kuimarisha TARURA ili iweze kutengeneza miradi mingi zaidi kadri inavyowezekana. Imani yangu ni kwamba fedha hizi ni pamoja na kuhakikisha kwamba tunajenga miradi mingi ya barabara ambayo inapunguza msongamano kwenye miji mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko barabara mbili muhimu sana kwenye Jimbo la Nyamagana, barabara ya kutoka Buhongwa kwenda Igoma na barabara ya kutoka Mkuyuni kupita Nyangerengere kwenda kutokea Mahina na Nyakato Buzuruga. Barabara hizi zikijengwa naamini kwamba TANROAD wangeweza sana kufanya kazi hii na TARURA sio eneo lake sana kwa sababu ukifikiria Nyamagana tunao mtandao wa barabara kilomita 738, lakini ni kilomita 47 peke yake ndio zimejengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama hatutazingatia msingi huu wa kuona maeneo muhimu tukaimarisha ujenzi wa barabara hizi, hatuwezi kusaidia chochote na badala yake tutakuwa tunaipa TARURA mzigo ambao haiwezi kuumudu kwa miaka yote inayokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sambamba na kwenye Jimbo la Ilemela ipo barabara ya kutoka Nyakato- Buseri - Monze yenye jumla ya kilometa 18. Leo tunakwenda mwaka wa tatu kilometa hizi toka zitengewe fedha imeshajengwa kilometa moja na point peke yake, sioni kama tuna dhamira njema ya kusaidia miji hii mikubwa ili iweze kupunguza msongamano na kuifanya ipumue kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo napenda kuzungumza ni juu ya uwanja wa ndege. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, toka tumeanza kuzungumza habari ya uwanja wa ndege wa Mwanza leo ni takribani miaka sita. Hivi malengo na mipango yetu ni ipi? Mimi nafahamu Serikali yenye dhamira ya kukusanya kodi nyingi kama Serikali ya Awamu ya Tano ina kila sababu ya kuimarisha maeneo ambayo ilikwishaanza. Ukiimarisha uwanja wa ndege wa Mwanza kabla hujakimbilia maeneo mengine mengi kwenda kushika huku na kule utakuwa umesaidia zaidi kuhakikisha eneo hili linaimarika kwa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuko asilimia 65 tunasema ya ujenzi wa jengo la abiria, ya ujenzi wa jengo la kuongezea ndege, uwanja wa kukimbilia kwa maana uwanja wa kurukia kwa maana ya runway, lakini tunajenga jengo kwa ajili ya mizigo. Hapa tunachokifanya ni sawa na kuvaa suti halafu unavaa kandambili; bila kujenga jengo la abiria hakuna tunachokifanya. Ni agizo la Mheshimiwa Rais viwanja vyote vinavyozunguka maeneo ya ziwa vijengewe cold room kubwa ambazo zitasaidia sana viwanja hivi kuwa kwenye maeneo ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko hata suala la ndege, unapozungumza kuimarisha Kiwanja cha Ndege cha Mwanza ndivyo unavyozungumza kuimarisha utalii wa ndani. Hata ndege hizi zinazozungumzwa hapa sana leo kwa hii robo peke yake nilikuwa najaribu kuona zaidi ya abiria 21,000 wamesafiri na ndege hizi ikiwemo Mwanza yenyewe kwa kiwanja chetu hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tafsiri yetu ni nini kukuza na kuendelea kuboresha uwanja wa ndege wa Mwanza itasaidia sana hata pato kubwa zaidi kuongezeka kwenye Serikali. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii atakuwa ni shahidi, kwa hii tu robo peke yake abiria hawa waliokuja Mwanza, wameenda Kigoma, wameenda Zanzibar, wameenda Bukoba, wameenda Comoro, wameenda Arusha, ni idadi kubwa sana ambayo inaingizia pato Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mpango wa Serikali ni nini? Niwaombe sana tuboreshe Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, kazi tuliyoifanya sasa Mheshimiwa Waziri itabaki kuwa haina maana kama hatutajenga jengo la abiria. Kinachozungumzwa hapa ni mkataba wa mkandarasi kuelekea mwisho, lakini ni bilioni 61 peke yake zimebaki, hebu tutoe hizi fedha tujenge jengo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini tukifanya hivyo tutafanya kazi kubwa, naomba nishukuru na tuone matokeo ya kazi ya Serikali ya Awamu ya Tano. Nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kupata nafasi ya kuchangia jioni ya leo. Kwa sababu ya muda, nianze moja kwa moja na hotel levy pamoja na bed night levy kwa maana ya tozo zinazotozwa na hotel za kitalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba Serikali yetu kupitia Mamlaka ya Serikali za Mitaa imejiwekea utaratibu wa kukusanya mapato kwa namna tofauti kwa misingi ya sheria. Katikati hapa kumekuwa na sintofahamu ya mwingiliano baina ya tozo ambazo zinatokana na bed night levy ambayo inatozwa na Bodi ya Hoteli za Kitalii ambayo imekasimiwa kwa TRA lakini halmashauri zinatoza hotel levy. Kumekuwepo na mkanganyiko ambao kwa muda fulani hivi umepelekea halmashauri hizi kupoteza mapato yake kwa namna fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Makatibu Wakuu wa Wizara hii ya Maliasili na Utalii lakini pia Katibu wa TAMISEMI. Nimezungumza nao na wamelichukulia suala hili serious na hivi navyoongea niwakumbushe na niwasisitize juu ya kuleta mabadiliko ya sheria hapa ndani ili kila mamlaka isimamie ukusanyaji sehemu inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili ni juu ya matumizi ya nishati ya mkaa na kuni. Imekuwepo kasumba au tabia kila hoja inayoibuka watendaji wanakwenda kutekeleza kwa namna wanayofikiri wao inafaa kuliko sheria inavyotaka. Hili limewakumba watu wengi sana, siyo tu Waheshimiwa Wabunge wanaotoka kwenye maeneo ya mijini lakini hata huko kwenye majimbo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Bunge hili halijawahi kutunga sheria ya kuzuia matumizi ya mkaa. Pia ni ukweli usiofichika, nimshukuru Waziri na Naibu wake, ukisoma katika ukurasa wa 37 wamesema vizuri kwamba zaidi ya asilimia 85 ya nishati yote nchini inatokanana na kuni na mkaa. Zaidi ya yote wamesisitiza wakasema takribani asilimia 90 ya wananchi wote hutegemea nishati hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sote tunafahamu wananchi zaidi ya asilimia 90 wanategemea nishati ya mkaa na kuni, inakuwaje leo mwananchi anayekutwa na baiskeli na pikipiki amebeba gunia moja, mawili anakuwa ni haramu katika nchi hii? Sote tunafahamu umuhimu wa matumizi ya mkaa na changamoto iliyopo. Mambo ya mabadiliko ya tabianchi ni lazima yaendane na muda huku tukimthamini mwananchi ambaye anawajibika kwenye hii asilimia 90. Mwananchi wetu wa leo asilimia 90 tunayoizungumza ni mwananchi ambaye anaijua leo yake na kesho yake haitambiui. Wananchi wengi kule tunapotoka, napotoka Nyamagana wapo wananchi wana uwezo wa kununua kifuko au kitini cha Sh.500 akatumia matumizi ya siku hiyo ili kesho yake ifike ajue kesho itakuwaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi navyozungumza na wewe tarehe 16 kwenye Kata ya Buhongwa kwenye maeneo ya Nyanembe, Nyangwi kwenda Bulola kule chini mpaka kwenye mpaka wa Misungwi mambo haya yanafanyika. Mambo haya yanatokea hata kwenye Wilaya nyingine za jirani za Magu na Kwimba. Waziri wananchi wananyanyasika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija Mwanza leo liko kundi kubwa la wafanyabiashara wanaouza kahawa, wako wa mama ntilie wanaotumia mikaa hii ili shughuli yao iende. Zaidi ya yote wako watu wanapika vitumbua. Sasa leo mtu anapika vitumbua akatumie gesi anaipata wapi? Mtungi mdogo wa gesi ni Sh.18,000, hiyo ni kujaziwa tu, ukienda kununua mtungi na gesi yake ni zaidi ya Sh.36,00. Gesi kilo 15 ni Sh.52,000 mpaka Sh.54,000, hiyo ni kujaza tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza vizuri, Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwenye hotuba amesema sawasawa muendelee kufikiria umuhimu wa kutengeneza mkaa mbadala. Wako wataalam wanasema kupitia taka zinazozalishwa majumbani unaweza ukatengeneza mkaa mbadala na ukasaidia. Mwanza peke yake Nyamagana kwa siku tunazalisha tani 350 za taka. Sasa ukienda pale dampo kwa mwezi tuna tani ngani, ni mkaa mbadala kiasi gani unaweza ukazalishwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri wakati wa kuhitimisha watujibu sawasawa matumizi ya mkaa yanaruhusiwa au hayaruhusiwi? Kama hauhusiwi mbadala wake ni upi ili wananchi wajue. Kama hatuna mbadala wa namna ya asilimia 90 ambao ni watumiaji wa mkaa na kuni wananchi wataendelea kunyanyasika na kukosa amani maana sasa baiskeli na pikipiki nyingi zimekamatwa. Hatujafika kwenye kiwango cha kuzuia matumizi ya mkaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huku amesema vizuri, ninukuu kidogo, Mheshimiwa Waziri amesema, wanaangalia namna bora ya kufundisha wananchi juu ya kutengeneza majiko banifu. Pia wamesema wanaangalia namna bora ya utaratibu wa kutengeneza au wa ulinzi wa misitu ya miti ya mkaa. Ulinzi huu lazima uanzie kule inakozalishwa mikaa. Juzi ameenda mtu mmoja pale kakuta mtu katandika mkaa wake, kaweka kwenye vitini kafunga na mikaa, hajakaa sawa anaingia ndani anatafuta mkaa ulipo anakamata, anatoka kwenye mkaa anatafuta na stoo anachukua mpaka uliopo stoo. Hii siyo sawa! Sijui mnanielewa maskini ya Mungu? (Makofi)

Hii siyo sawa Mheshimiwa Waziri. Ni lazima tuhakikishe watendaji tunaowatuma kufanya kazi hii wanaifanya kwa weledi na ubora tukihakikisha maisha ya Watanzania tunaendelea kuyalea ili waendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine amesema watahakikisha wanafundisha mbinu mbadala lakini kuangalia maeneo maalum yatakayokuwa yanauziwa mikaa hii. Hili jambo lifanyike mapema na ijulikane mikaa yote itakuwa inanunuliwa sehemu fulani. Mwanza tuna Kata 18 tuambiwe kata zipi na zipi, kama ni za mipakani, kama ni za katikati ili mikaa hii ipatikane na mwananchi anayekutwa na gunia moja asiwe haramu au haramia, tukifanya hivyo itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lazima tuseme, Waziri ametuambia yuko tayari kutambua wauzaji wa mikaa, inachukua muda gani kutambua wauzaji wa mikaa, wako wengi, wako wakubwa, wa kati na wadogo. Wale wakubwa ndiyo wanagawa kwa wadogo huku. Mama mwenye maisha yake ya kawaida mjane ana uwezo wa kuuza gunia moja likiisha anaongeza lingine. Lazima tuwaonee huruma watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho amesema wataangalia namna bora ya kuhamasisha ili taasisi nyingi zinazotumia mkaa zielimishwe juu ya matumizi haya. Nishauri siyo tu kuelimishwa, waelimishwe zaidi taasisi hizi juu ya kupanda miti kabla ya kuikata itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka leo nijikite sana kwenye mkaa kwa sababu napotoka ndipo kuna wauza kahawa wengi, wapika vitumbua wengi na mama lishe wengi, wote hawa wanatumia nishati ya mkaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini sio mwisho kwa umuhimu, niwapongeze sana watendaji wote wa Kituo cha Saanane. Mheshimiwa Waziri nimkushukuru sana, leo tunazungumzia watalii wanaokwenda kwenye kituo Saanane wapatao 12,600, hii siyo idadi ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamefanya kazi kubwa, wameboresha njia na wameboresha kila namna ya kuvutia watalii. Naomba watuimarishie uwanja wetu wa Mwanza ili kwenda sambamba na utalii huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana nami kupata nafasi angalau ya kuchangia mchana huu maneno machache juu ya Wizara hii muhimu kabisa katika maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini niwapongeze sana na nianze na pongezi kwenye Wizara hii. Nimshukuru na nimpongeze sana Waziri wa Ardhi pamoja na Naibu wake, pamoja na Watendaji wao wote kwa namna ya kipekee wanavyofanya kazi lakini kwa ubunifu wa hali ya juu ambao wamekuwa wakiuonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu watakubaliana na mimi, kwa mara ya kwanza safari hii tumeona maonyesho makubwa hapa ndani ya Bunge yanayoendana sambamba na taasisi mbalimbali za kifedha ambapo kwa maana ndogo kabisa sisi Wabunge tumepata fursa za kujua vitu ambavyo pengine ingetuchukua zaidi ya siku nyingi kupata fursa ya kwenda kwenye benki, taasisi hizi za National Housing, sijui Watumishi Housing na nyingine nyingi kujadili na namna ya kuona namna ya upatikanaji wa mikopo ya ujenzi wa nyumba zenye gharama nafuu, mimi niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niongelee kuhusu Nationa Housing. Nitumie nafasi kuiomba sana Serikali; tunafahamu National Housing Serikali imewekeza fedha nyingi na msingi wake mkubwa ni kuendeleza Shirika hili liweze kujitegemea. Vile vile iko miradi na Kamati imesema vizuri, miradi mingi mikubwa, mizuri, imefanyika kwa muda mrefu na mingine imesimama fedha bado hazijakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaiomba sana Serikali waliunge mkono Shirika hili ili liweze kutimiza wajibu wake kama ambavyo limejipangia na namna ya kutekeleza shughuli nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika 10 ni chache sana, nizungumze sasa juu ya habari ya urasimishaji na umilikishaji wa ardhi. Nirudie tena kusema nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya. Jiji la Mwanza pamoja na Manispaa ya Ilemela na Nyamagana tumekuwa watu wa kwanza katika nchi hii, hivi ninavyozungumza tumeshapima viwanja zaidi ya 42,563.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika idadi hii ya viwanja zaidi ya hati 13,202 zimeshakabidhiwa kwa wananchi. Nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Watendaji wa Ardhi wa Manispaa ya Ilemela pamoja na Jiji la Mwanza kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya ya kuwahudumia wananchi wa maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya Serikali kupitia mpango ambao waliuanzisha Dar es Salaam na Wizara ikatoa fedha kwa ajili ya manispaa fulani, sitapenda kuitaja jina ili itekeleze mpango wa urasimishaji makazi, kwenye Kitabu cha Mheshimiwa Waziri amesema wamepima viwanja 6,000 wametoa hati 170 peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu Nyamagana na Ilemela wamefanya kazi kubwa, tunaomba Mheshimiwa Waziri awaunge mkono kwa kuwaongezea fedha nyingi zaidi ili waweze kufanya kazi hii kwa umakini kubwa na wasiendelee kusuasua kama ambavyo wanajitahidi sasa pamoja na kazi kubwa sana hii wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo lingine juu ya namna nzima ya kushughulika na masuala ya utoaji katika suala nzima la umilikishaji. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, alipunguza ile gharama ya premier kutoka 7.5 mpaka 2.5 na sasa Kamati imeomba angalau iwe one percent, nami niendelee kusisitiza hapo aiangalie kwa upana na aweze kuona namna ya kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, program ya ununuzi wa vifaa vya upimaji; Mheshimiwa Waziri ameongea kwenye Ukurasa wa 36, ni jambo nzuri sana kwa sababu atapunguza gharama za upimaji wa maeneo mengi kwenye manispaa zetu na halmashauri zetu. Hii itamsaidia mwananchi kulipa gharama nafuu sana ili sambamba na wakati tulionao sasa aweze kupima maeneo mengi zaidi. Vile vile kila Mwananchi apime akiwa na uhuru mkubwa ili aweze kujisaidia wakati fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri ahadi hii itekeleze. Nafurahi kuona na nimpongeze tena, amesema mwezi wa Saba tunapoanza mwaka mpya wa fedha, fedha hizi na vifaa hivi vitakuwa vimeshapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Master Plan, nchi hii imekuwa ikitengeneza Master Plan nyingi, imekuwa ikitengeneza michoro mingi, lakini Mheshimiwa Waziri hakuna mpango mkakati wa kuhakikisha Master Plan hizi zinatekelezeka kwa wakati na matokeo yake tunaendelea kuchochea migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna nyingine, kama Master Plan hizi hazitafanya kazi kwa haraka, utekelezaji wake ukawa nyuma hatuwezi kufanikiwa kwenye malengo tuliyoyakusudia. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri tuweke msisitizo na tuimarishe maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ni kwenye mpango mkubwa ambao tunaufanya sasa wa mpango wa miji mikubwa. Kwenye miji yetu mingi tunayo changamoto moja kubwa, mpango kabambe ni mzuri, lakini hebu tuangalie, wako wananchi kwenye maeneo fulani hawawezi kupimiwa na kupewa hati zao. Sasa hii itakuwa ngumu sana kwa mwekezaji anayekuja kuja kukutana na mtu ambaye si mmilikia halali, hana document ili aweze kumiliki eneo lile na kwenda sambamba na mpango kabambe tuliouandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala litatukwamisha; yako maeneo ya Kata za Isamilo karibu mitaa nane na mitaa mitano kwenye Kata ya Mbugani pale kwenye Jimbo la Nyamagana. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aangalie na wajadiliaje vizuri, waone namna ambavyo tunaweza kumsaidia mwananchi huyu kwenye Kata hizi mbili za Mbugani na Isamilo ili naye awe kwenye mpango kabambe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa miaka mitatu. Ni ukweli usiopingika kwamba Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Wasaidizi wake imefanya kazi kubwa sana kwa kipindi hiki tulichonacho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli ule ule usiopingika Mheshimiwa Waziri wa Fedha amefanya jitihada kubwa sana, kila ambayo tulidhani tunaweza kuyafanya toka tulipoanza, tumeyafanya kwa sehemu yake kwa kiasi kikubwa sana. Haitakaa itokee na haitawezekana kila linalofanyika na Serikali watu wakalisema vizuri, hasa wanapoitwa Wapinzani. Nianze kwa kuishukuru Serikali, moja kati ya mipango ambayo inatazamia kuifanya ni kuhakikisha nchi yetu na miji yetu yote mikubwa inapimwa, inapangwa, inarasimishwa na kuhakikisha Watanzania hawa wanaondokana na wimbi la umasikini ikiwa ni moja ya kipaumbele, lakini ikiwa ni sehemu ya kuongeza thamani ya ardhi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Wizara ya Ardhi imefanya kazi kubwa sana, hasa kuhakikisha ardhi kubwa inapimwa lakini kuendelea kukagua mipaka na kuweka mipaka ili kuonyesha maeneo yanayostahili kutumika na yasiyostahili. Maeneo yote ya miji ambayo yametengenezewa mpango kabambe yanazo changamoto kubwa. Ukichukua kwenye miji mikubwa, kwa mfano, Mwanza ni moja kati ya mji ambao umetengenezwa kwa ajili ya mpango kabambe lakini huu mpango kabambe unaenda sambamba na urasimishaji wa makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaofanya zoezi la urasimishaji wa makazi ni Halmashauri. Nami naiomba sana Serikali, Halmashauri zetu peke yake haziwezi kufikia kiwango tunachokitegemea kama Wizara. Ni vyema sasa Serikali ikaangalia uwezekano wa kuwekeza fedha. Nami niwapongeze, Serikali imenunua vifaa kupitia Wizara kwa ajili ya upimaji, hii ni hatua kubwa sana. Vifaa hivi vikitumika vizuri, Wizara ikiwezeshwa, Halmashauri zikawa zinapewa kazi ya kupima maeneo na tukatengeneza mipaka zitaondoa migogoro ya ardhi ambayo bado ni mikubwa sana kwenye nchi hii. Kwa namna tunayoendanayo, hatuwezi kumaliza kwa wakati na migogoro itaendelea kuwa mikubwa kila leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukizungumza kwenye mpango mkakati wa upangaji miji, chukulia mfano wa Mwanza, ni mji ambao umeinuka, una milima mingi, yako maeneo bado hayatakiwi kupimwa. Unapozungumza kuweka mkakati wa kuboresha maeneo, wanapokuja wadau kushiriki kwenye ule mpango, wanapomkuta mwananchi hajamilikishwa hili eneo, bado hana haki ya lile eneo na kipande ambacho amekiishi zaidi ya miaka 40. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali, moja ya mkakati ni kuhakikisha maeneo yote yanayotakiwa kurasimishwa kwenye miji yapimwe, yarasimishwe na wananchi hao wakabidhiwe hati. Kwanza, tunaongeza thamani ya eneo lakini pili tunamtambua mmiliki ambaye ametusaidia kutunza eneo hilo zaidi ya miaka 40. Haya yamejitokeza Nyamagana kwenye Kata zaidi ya tatu, Igogo, Nyachana, Mbugani, Isamilo, Mabatini na nyingine nyingi pamoja na miji mingine yote mikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine napenda nishauri, tumezungumza habari ya viwanja vya ndege. Ni kweli kabisa tunatamani kila sehemu kuwe na kiwanja cha ndege ikiwezekana. Nami nashukuru sana, nataka niishauri Serikali, viwanja ambavyo viko kimkakati tuvipe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, unapozungumzia uwanja wa ndege wa Mwanza, uwanja ule uko kimkakati. Haiwezekani leo tuna miaka sita tunauangalia tu hatutaki kuujenga uwanja ule kwa kiwango kinachostahili. Leo tuko 70% upande gani? Ni majengo ya abiria, running way, jengo la mizigo au ni controlling tower? Kwa hiyo, ni lazima tuhakikishe tunaweka kipaumbele kwenye mambo ambayo tunatazamia yatazalisha matokeo makubwa ili Serikali iweze kupata kipato kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho napenda kuchangia ni juu ya sekta binafsi katika utekelezaji wa viwanda vya ndani. Ni kweli naunga mkono, ni vyema kila mkoa ukawa na hivyo viwanda 100, nami napongeza sana na Wakuu wa Mikoa wamefanya kazi kubwa lakini hivi viwanda 100 vina uwezo wa kuajiri mtu 1 mpaka 5. Dhamira yetu sisi tulioko kwenye miji mikubwa tunavyo viwanda vya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Mwanza tuna viwanda vya samaki. Namshukuru Mheshimiwa Dkt. Mpango amesisitiza kuhakikisha tuna viwanda vinavyotumia malighafi ya ndani. Viwanda vya samaki vya Mwanza malighafi ya ndani ni samaki, operesheni imepita sasa hivi mazao ya samaki ni makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ni lazima tukubaliane kwamba bila kuvipa uwezo viwanda hivi, ambavyo mnyororo wake ni mkubwa, vitaajiri watu wengi lakini vitaongeza ukuaji wa kipato kwa kila mtu mmoja mmoja kuanzia mvuvi, mchuuzi mpaka uuzaji mkubwa. Ndiyo maana tunazungumza habari ya kiwanja cha ndege, tunazungumza habari ya ujenzi wa meli na kuboresha meli nyingine zote zilizopo. Tukifanya hivyo itatusaidia sana. Lengo ni lazima tuwe na kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nawashukuru sana Wizara ya Afya, wamefanya jambo moja zuri sana kupitia TAMISEMI. Kila Kituo cha Afya kinachotakiwa kujengwa kinapelekewa fedha zake, kama ni shilingi milioni 500 au ni shilingi milioni 400 na wanaamua tunataka kujenga vituo 200, vinajengwa 200 kwa wakati na vinakamilika. Sasa haya ni lazima tuenende nayo katika kuhakikisha tunausaidia umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maneno kwamba vitu tunavyovifanya haviwasaidii watu siyo kweli. Hivi leo unataka kuniambia zahanati zinazojengwa haziwasaidii wananchi wa kawaida? Zinawasaidia akina nani? Kwa hiyo, ni lazima tukubali, kupanga ni kuchagua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Mwakajoka pale amesema, nchi hii tumepewa wote, lakini aliyepewa nchi hii sasa hivi kuhakikisha anaishughulikia, anaijenga sawasawa ni aliyepewa dhamana, ni Chama cha Mapinduzi. Hiki ndicho kina dhamana ya kuangalia wapi kuna tatizo na wapi hakuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumechagua kupeleka maji, kujenga hospitali, kupeleka dawa, kutengeneza barabara, meli na standard gauge na haya ndiyo mahitaji ya wananchi. Leo Waheshimiwa Wabunge mniambie nani kwenye mikutano alishawahi kuulizwa suala la Katiba? Binafsi sijawahi kuulizwa swali la Katiba na nimekuwa na mikutano zaidi ya 1,000, wananchi wanauliza maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunapozungumza Katiba, niulize humu ndani leo mnisaidie, nani anaitaka Katiba? Ni mwananchi, mwanasiasa au nani mwingine? Sote tunajua, sisi wanasiasa ndiyo tunataka Katiba kwa sababu tunataka dola, tunataka madaraka. Utafika wakati tutajua ni wakati gani tubadilishe Katiba kwa manufaa ya Watanzania na wakati gani tuendelee mbele? (Makofi)

(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliongea bila mpangilio)

Kwa hiyo, hizi nyingine ni porojo na kelele nyingi haziwezi kutusaidia. Nachoamini, Watanzania wengi leo kila unayemgusa anataka yatokanayo na maendeleo, mambo yanayotatua changamoto zake za kila kunapokucha. Huo ndiyo msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Napenda sana kwa nafasi hii nami nichangie walau maeneo machache ambayo nadhani nitayasemea vizuri kwa ajili ya faida na manufaa ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba nami sitakuwa nyuma kuungana na wenzangu wote walioipongeza na kuishukuru Serikali kwa utendaji wake mkubwa ambao kwa kweli unaonekana kwa vitendo na si kwa maneno peke yake. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu namna ambavyo amekuwa akishiriki kwa asimilia kubwa kuhakikisha majukumu yote ya Wizara anayoisimamia yanatekelezeka kwa wakati na kwa namna ambavyo yamekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda njikite kwenye mambo ambayo nimepanga kuyazungumzia sana. Moja ni juu ya viwanja vya ndege. Ni ukweli usiofichika kwamba Taifa letu sasa hivi baada ya kuwa lina uwezo wa kumiliki ndege ilizonazo leo hakuna ukweli unaopingika kwamba ni lazima sasa tujikite kwenye kuimarisha viwanja vyetu vya ndege. Tumeanza ujenzi wa viwanja hivi kwa muda mrefu, vingine vilihitaji ukarabati mdogo, vingine vilihitaji ukarabati wa kati na vingine vilihitaji ujenzi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila wakati nimekuwa nikisema juu ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Uwanja huu kwa namna ulivyoanza na unavyopangiwa bajeti kila kukicha lakini bajeti hii isipokamilika kama ambavyo imekuwa, leo tuna zaidi ya miaka ya sita tunazungumzia uwanja wa ndege ambao unasafirisha abiria wengi kabisa kwenye nchi hii. Mwaka jana nilisema hapa na hata Mheshimiwa Waziri wa Utalii atakuwa ni shahidi yangu. Ushahidi huu unatoka na ubora na umuhimu wa Uwanja wa ndege wa Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rekodi tulizokuwa nazo mwaka jana kama tutaendelea hivi tutamaliza miaka hii uwanja huu hautafanikiwa. Tumeshajenga jengo la mizigo, jengo la kuendeshea ndege na tumeshapanua uwanja wa ndege, kila siku nasema huku ni sawa na kuvaa suti na kutembea na kandambili hutaonekana nadhifu kwa sababu ya namna ambavyo unaonekana. Kwa hiyo, nishauri sana Serikali kwa bajeti hii ambayo tumeitenga safari hii, Mheshimiwa Waziri Mkuu Uwanja wa Ndege wa Mwanza uwe ni sehemu ya kipaumbele tukiwa tumeelekeza katika kukuza utalii, lakini tukiwa tumeelekeza katika kuendelea kulipa hadhi Shirika letu la Ndege lakini ubora wa kiwanja chenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nilitaka nizungumzie juu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Tulipoamua kuikabidhi Mamlaka ya Mapato Tanzania jukumu la ukusanyaji wa mapato kwenye maeneo mbalimbali kutoka Halmashauri kuna mambo ambayo yatatupelekea miaka inayokuja tupoteze kabisa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka kwenye Jiji, pale katikati Mwanza Mjini, leo ushuru wa mabango baada ya kwenda TRA, naamini tukiwaweka hapa watupe record, record watakazotupa hazitalingana na kile ambacho kilikuwa kinafanywa na Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaweza kupigwa mkono gari mfano gari ya Pepsi, gari yenye trela ikipigwa mkono inachukuliwa futi inapimwa urefu na upana mtu anatozwa shilingi 500,000, shilingi 600,000 au shilingi 800,000 kwa gari moja, ana gari 300 huyu mtu, unategemea makampuni ya stahili hii yatafanya nini? Yalichoamua sasa hivi ni kufuta maandishi wanabakisha rangi nyekundu, Pepsi atafuta maandishi ya Pepsi atabakisha rangi ya blue na Konyagi watafuta konyagi watabakisha rangi za njano. Matokeo yake ni nini? Mwaka ujao hatutapata hata shilingi 100 ya fedha kidogo ambayo tungeweza kuipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe warudi nyuma ambavyo Halmashauri zilikuwa zinafanya. Mfano upo, Mheshimiwa Rais alipoelekeza kukusanya kodi ya majengo kwa kiwango cha shilingi 10,000 na shilingi 50,000 kwenye nyumba zenye sakafu moja na kuendelea imeleta mafanikio makubwa sana. Kwa nini hawataki kujifunza kufanya kidogo ili upate kingi? Sasa ni sehemu ambayo inatupa tabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu suala la vitambulisho na namshukuru Mheshimiwa Rais amelisema juzi. Yuko mwendesha bodaboda ambaye tayari ameshatambuliwa na Serikali, ndiyo maana leo analipa bima Sh.76,800, leseni ya pikipiki shilingi 56,000, kodi ya Halmashauri ambayo wanagawa 50% na SUMATRA shilingi 22,000, tunapomwambia leo alipe Sh.20,000 tunamkosea na tunamkosea Mheshimiwa Rais kwa sababu siyo sawa. Ni lazima tuwaache hawa watu walipo na tuangalie namna ya kuwapunguzia mzigo na siyo kuendelea kuongeza mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumza juu ya uboreshaji wa bandari. Sisi sote hapa tunafahamiana na sote hapa tunafanya biashara kwa namna moja au nyingine. Bandari ya Da es Salaam pamoja upanuzi mkubwa tunaoufanya leo hatuwezi kufanikiwa kwa sababu ya namna mbovu inavyoshughulikia ukusanyaji mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo haya tusipoyasimamia, mtu ana bonded warehouse, huyu ni mtu anauza brands ikifika wakati brands zimeisha huyu mtu anaonekana lazima alipe kodi wakati ambao sote tunafahamu namna anavyokwenda. Lazima tukubali tunapoboresha hizi bandari leo tunataka ku-archive nini? Kazi ya mtu wa TPA ni nini? Kazi ya mtu wa Mapato ni ipi? Ni lazima tukubaliane haya mambo yaende kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimependa sana nizungumze juu ya habari ya Mifuko yetu hii ya Hifadhi ya Jamii. Nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Wakurugenzi waliopata nafasi hizi, Mkurugenzi wa PSSSF, Ndugu yangu Kashimba na Ndugu yangu Erio wa NSSF. Tunaamini baada ya migogoro mingi na wanafanya kazi kubwa sana, huu ni wakati wao sasa wa kuhakikisha ule umuhimu wa Serikali kuyaunganisha unaonekana kwa kutoa huduma bora. Kwa uwezo na sifa zao na kuwa kwenye sekta hii kwa muda mrefu sina shaka watafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mwisho, Limezungumzwa humu, na mimi naomba hili niliseme kwa masikitiko makubwa sana. Wizara hii jukumu lake na Wizara kupitia sekta hii ya Mambo ya Ndani kupitia sekta ya Uhamiaji, kuna mdau mmoja amekuwa anasemwa sana humu ndani na kila akitaka kusemwa sisi tunaguswa. Bahati nzuri Mheshimiwa kila akitaka kuongea anasema najua wako watu humu wataumia.

Mimi ni mmoja watu wanaoumia, naomba nikiri hivyo. Kwa sababu mtu huyu ni mwekezaji, haijalishi ameishi hapa miaka mingapi. Kutaka kupata leo uraia siyo jukumu la Wizara kusema apewe au asipewe. Jukumu la Wizara ni kuhakikisha haki na utaratibu na sheria zimefuatwa. Leo mtu akitaka kuomba uraia kutumia utaratibu anaambiwa amehonga pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nilitegemea sana Mheshimiwa Waziri aombe hapa kama kuna ushahidi unatumika kama huyu mtu ni mhalifu kwanini asishughulikiwe?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa. Ahsante sana Mheshimiwa Mabula. Mheshimiwa Mabula, muda wetu ndiyo huo.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuweza kuchangia walau maneno machache ya kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kutoa shukurani zangu za ujumla kwa Mheshimiwa Jafo pamoja na watendaji wenzake wote kwenye Wizara kwa namna ambavyo wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana katika kuhudumia Wizara hii nyeti kabisa kwenye nchi hii. Mimi nilitegemea sana kwa sababu TAMISEMI ndiyo kiini au injini ya maendeleo kwenye nchi hii hata Wabunge wenzetu wote wangeendelea kuona umuhimu wa kukupa moyo na kuendelea kukushawishi na kuendelea kukueleza maeneo ambayo wanadhani yanatakiwa kufanyiwa kazi badala ya kuendelea kulalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuzungumzia sekta ya afya. Nafahamu Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa sana. Mimi natoka Jimbo la Nyamagana. Naposema Nyamagana unafahamu ndiyo kitovu cha Mkoa wa Mwanza. Tunashukuru sana kwa mgao wa vituo vingi vya afya na Nyamagana tunacho kituo kimoja cha afya chenye sifa ambacho umetupa sasa hivi kimeshakamilika. Nikushukuru tena kwa kutuongezea kituo cha pili kule Fumagira. Imani yangu ni kwamba kituo hiki kikikamilika tutakuwa tumeendelea kupunguza sana tatizo la vifo vya mama na watoto ambao kiukweli wanahitaji huduma za karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi Halmashauri peke yake, nimpongeze sana Mkurugenzi wangu pamoja na watendaji wote, Madiwani na Meya kwa kuhakikisha tunajenga zahanati sita mpya kwa fedha za mapato ya ndani. Hii ni hatua kubwa sana na tunaposema Hapa Kazi Tu, hii ndiyo tafsiri yake sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo moja kubwa ambalo Mheshimiwa Waziri inabidi sasa hivi ukimbie nalo, baada ya ujenzi wa hivi vituo vya afya vyote na hospitali za wilaya, jambo kubwa tulilonalo sasa ni upatikanaji wa vifaa. Tunafahamu vinatoka kwa awamu, sasa hivi vimeanza kwa awamu ya kwanza lakini umekwenda karibia phase nne ya ujenzi wa vituo vya afya. Kwa hiyo, ni jambo zuri sana tukifanya haya mambo kwa haraka ili wananchi waone matokeo tunayoyasema kwa vitendo kama ambavyo umeshaanza kupeleka vifaa kwenye vituo vingi vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwa sababu ya muda nizungumze juu ya TARURA. Mheshimiwa Waziri katika jambo ambalo naendelea kukupongeza sana kila siku ni uamuzi wako wa kutoa mawazo na Baraza likaazimia na Mheshimiwa Rais akaidhinisha kuwa na chombo kinachoitwa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema mimi ni muumini mkubwa wa TARURA kwa sababu nimeona matokeo yake lakini najua namna ambavyo TARURA inaweza kuja kuwa mkombozi wa miundombinu ya barabara kwenye nchi hii hasa kwenye maeneo ya vijijini na mjini. Juzi nimesikia wakati unazungumzia hapa ripoti ya CAG, TARURA wamepata hati safi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mkurugenzi/CEO wa TARURA Ndugu yangu Seif pamoja na Mhasibu Mkuu Ndugu yangu Nyaulinga kwa namna ambavyo wamekuwa wakishirikiana vizuri na watendaji wao wote hata kupata hati safi. Endelea kuwawekea mkazo, zaidi ni kuhakikisha fedha zinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nyamagana napata shilingi bilioni 3.5 lakini fedha hizi ukilinganisha ukubwa wa mji na sifa ya mji na miundombinu iliyopo hatujawahi kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara za lami. Hatuwezi kuendelea kujenga au kuboresha barabara za vumbi. Kwa hiyo, niwaombe sana Watendaji wa TARURA waangalie kwenye kitengo cha barabara za lami kwenye Jiji la Mwanza tutakapoongeza barabara za lami walau kutoka Igoma - Buhongwa, kutoka Mkuyuni kwenda Mandu kupitia Mahina, kutoka Buhongwa kwenda Nyakagwe na kule Bulale tutakuwa tumefungua mji huu na sifa yake itaonekana. Mimi sishangai sana kwa sababu haya mazuri tusipoyasema leo tutayasema lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Madiwani, nimekuwa Diwani na nakubaliana na suala la posho zile za mwisho wa mwezi, Serikali inaendelea kulifanyia kazi. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri umetoka Waraka unaosisitiza sitting allowance, Mheshimiwa Diwani anayetoka kilometa 18 anakuja kulipwa Sh.10,000 ya nauli, hii siyo sawa. Maelekezo kwenye Waraka yako wazi kwamba Diwani apewe malipo haya kulingana na uwezo wa Halmashauri inavyokusanya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo kwenye Halmashauri kama ya Jiji la Mwanza na Mkurugenzi wangu hawezi kutumia nguvu kwa sababu Waraka umemuelekeza kutumia Sh.40,000 na Sh.10,000. Mheshimiwa Waziri, fungua sasa kwamba Halmashauri itoe posho ya kikao kwa siku kulingana na uwezo wake wa mapato ya ndani. Ukifanya hivi, mwanzo walikuwa wanalipwa Sh.100,000 na mimi nilikuwepo pale tunalipwa Sh.100,000 ukija kwenye kikao, nauli na kadhalika angalau unaweza kuhudumiwa hata wapiga kura wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo, najua bado nina dakika tano baada ya kengele hii, yako maneno mengi yanaenea kwenye hii nyumba. Mimi niwasihi Waheshimiwa Madiwani yako maneno yanasema ashindwaye haishi maneno lakini sote tunafahamu hapa tunapokuja kujadili bajeti na bajeti tunayokwenda kuijadili tunafanya makisio. Hivi leo ukikisia kupata Sh.10,000 ukaishia kupata Sh.8, unamlaumu nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishia kulaumu bajeti tunayoipata, hatuoni mambo ambayo Serikali imefanya. Kila mtu akisimama wanabeza Stiegler’s Gorge na ndege lakini wanasahau Serikali ya Awamu ya Tano kutoka wanafunzi wa vyuo vikuu 30,000 mpaka 42,000, zaidi ya shilingi bilioni 420 zimetoka hapa. Hili siyo jambo jema la kushukuru ndugu Waheshimiwa wa upande wa kule? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niulize, tunasema hivi kutoka miundombinu kwenye zaidi ya shule 500, zaidi ya shilingi bilioni 100 zilizofanyiwa ukarabati na kujengwa hili siyo bora kuliko yale mengine tunayoyasema? Tumezungumza hapa tunasema, hivi leo unapozungumzia ujenzi wa vituo vya afya zaisdi ya 300, hospitali za wilaya zaidi ya 67, unabeza hata hili? Hatuoni haya? Tunajadili mipango ya kufikirika…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwakajoka kaa nitakushukia jumla jumla.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapojadili habari ya bajeti, bajeti ni matarajio. Kama tulipanga kufikisha shilingi bilioni 1 tukaishia shilingi bilioni 2.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 vyama vya upinzani viliundwa, malengo yao ni kuchukua dola. Kama ingekuwa ukifikiri unatenda, leo wangekuwa wamechukua dola wale.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania siyo kijiji. Tanzania ni duara, ni nchi kubwa na wanakosea sana kuilinganisha Tanzania na vijiji. Wanakosea sana kuilinganisha Tanzania na mtaa. Hii ni nchi, ina wilaya, mikoa na ardhi kubwa na watu zaidi ya milioni 50, inataka mipango na mipango hii inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, tunaamini kuja mpaka mtukamate hapa tulipo ni kazi ya ziada sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana lakini waendelee kujifunza. Kwa mfano, kwa kumalizia, tumesema hivi toka nchi hii umeundwa kwa mara ya kwanza maamuzi ya ujenzi wa Bwawa la Stiegler’s Gorge tunataka wananchi watoke kwenye kulipa senti 11 ya umeme tunayolipa leo waje walipe senti 5 au 6. Mtu mwingine anasema hapana, huyu mwananchi unayetaka aendelee …

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Azimio la Kufuta Hasara itokanayo na Maduhuli ya Madeni ya Nyuma ya Ada na Leseni za Magari, Riba na Adhabu kwa kipindi kinachoishia tarehe 30 Juni, 2019
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia walau kidogo. Kwanza naunga mkono Azimio la kufuta na kusamehe hasara ya maduhuli ambayo Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Waziri wa Fedha mwaka 2017/2018, wakati Waziri wa Fedha anakuja hapa kuwasilisha bajeti yake, moja ya jambo kubwa lilikuwa ni kufuta leseni za magari ambazo zimekuwa na usumbufu mkubwa na kero kubwa sana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni jambo ambalo kila mmoja ndani ya nyumba hii alipiga makofi na kulishangilia kwa sababu siyo tu liliwahusu watu walioko nje ya nyumba hii, lakini hata sisi miongoni mwa Wabunge tuliopo ndani ya jengo hili tulifaidika na msamaha wa huu kodi na maduhuli haya mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni jambo tu la kushangaza na ndipo huku tunapoanza kufahamiana siku zote kwamba sio kila jambo linastahili kupingwa. Tunaongelea kodi ya shilingi milioni 398, wadaiwa waliokuwa wanadaiwa fedha hizi ni zaidi 365,600. Kwa hiyo, hata ukifanya hesabu ya kawaida sio zaidi ya shilingi milioni moja walikuwa wanadiwa kila mtu ambaye amesamehewa deni hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lazima tufike sehemu tukubali, mimi nikiri kazi nzuri iliyofanywa na Serikali, maelekezo mazuri yaliyofanywa na Wizara ya Fedha kwa kuleta hoja Bungeni na sisi kama Wabunge tukaipokea na kuifanyia kazi. Kazi kubwa iliyofanywa na Kamati kwa niaba ya Bunge ni kupitia na kujiridhisha Mkaguzi wetu ambaye ni jicho amefanya kazi yake sawasawa? Kama kamati yako imejiridhisha bila shaka kwa maelekezo na maandishi ya Mheshimiwa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) tena wakati huo Mheshimiwa Peter Serukamba amesema vizuri dokezo hili limesainiwa na Ndugu Profesa Assad mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa lazima tukubaliane hoja hii tunayoiongea mimi nitoe pongezi kwa Serikali nikupngeze sana Waziri wa Fedha na timu yako kwa kuamua kutuonesha Watanzania huu ndio mfumo wa utawala bora tunaouzungumza katika kujenga na kutetea maslahi ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tukubaliane, Mwenyekiti wangu pengine ameteleza, sote tunafahamu hakuna gari la Serikali ambalo linalipiwa kodi. Kodi tunayozungumza hapa ni kodi ambazo sisi kama wananchi tunapoingiza magari tunafanya utaratibu wa kulipa leseni na baadaye tumekuwa tukiendelea hivyo. Lakini mimi niseme ni lazima tujifunze kushukuru hata ambapo hatutamani kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kusema jambo hili ni kubwa na mimi niombe jambo moja Mheshimiwa Waziri huko mbele tunakoenda hizi hoja ambazo zinachafua vitabu kwenye mahesabu, hoja za muda mrefu tuangalie pia mbali na kwenye Halmashauri zetu zipo hoja za muda mrefu zaidi miaka kumi. Sasa tuangalie utaratibu mzuri, CAG awe anazifuta kwa utaratibu huu hii nchi tutaijenga tena tutaijenga sana sana na tutendelea kuwepo sana kwa style hii kama ndio hali yenyewe hii Mungu akubariki sana Mzee Mipango pamoja na msaidizi wako kazi nzuri sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia walau machache kwenye hii Wizara muhimu kabisa, Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nijikite kwenye mambo machache ambayo kwa kweli nadhani yananipa deni sana kama sitayazungumza. Jambo la kwanza, wiki chache zilizopita nilizungumza juu ya masuala ya minada. Tunafahamu, kuna minada ya upili na minada ya msingi. Sasa miaka michache iliyopita Wizara iliamua kwa kukaa tu na kufikiria bila kuwa na sheria ambayo ingeweza kutuongoza vizuri, kwamba kwa sababu yako baadhi ya maeneo yana minada iliyokuwa inaendelea ilikuwa imejaa sana, sasa wakaamua kuhamisha ile minada kupeleka kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya sana watu wa Nyamagana na Ilemela kule minada yao ya msingi ikaondolewa na kupelekwa Misungwi ambapo wakaenda kuanzisha mnada wa upili. Matokeo yake ni nini; kuhamishwa huku kwa minada kulitokana na sababu za msingi tu kwamba maeneo ya awali yaliyokuwa yanatumiwa kwa minada, kama pale Nyamagana tulikuwa na eneo pale Igoma, kwamba eneo hili limekuwa finyu sana kwa hiyo ni lazima tuhamishe mnada. Hii imefanyika pia Pugu kwenda Ruvu na sisi tukatoka Nyamagana kwenda Misungwi.

Mheshimiwa Spika, lakini hoja yangu hapa ni nini; kulikuwa na sababu gani ya kuuhamisha mnada Nyamagana ukaenda Misungwi ilihali ule mnada ungeweza kutoka eneo ulilokuepo awali ukapelekwa kwenye eneo lingine. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri; sisi Nayamagana tuna eneo mbadala la zaidi ya ekari 35 mpaka 50, linatosha kwa ajili ya kupata mnada mpya wa msingi ambao utakuwa Nyamagana ili tuondoe hizi kero na changamoto tunazoziweka kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, nilisema hapa mfugaji au mchinjaji anakwenda kununua ng’ombe Magu, analipa 7,500 anapewa kibali kwenda Misungwi, anatoka Magu anapitiliza mpaka Misungwi, anafika Misungwi analipa 7,500 ndipo anapewa kibali kutoka Misungwi kuja kuchinja ng’ombe Nyamagana, hii siyo sawa. Tunaongeza mzigo kwa wavuvi, tunaongeza mzigo kwa wachinjaji na hatutawasaidia sana. Kwa hiyo niombe sana Wizara kwa sababu mlishaanza kulifanyia kazi, tunaomba mnada wetu uliokuwa unatakiwa urudi Nyamagana urudi ili tuweze kuendelea na shughuli za uchinjaji na mapato ambayo yaliyokuwa yanapotea kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, la pili; tuna kiwanda cha ngozi pale Mwanza kinaitwa Mwanza Tanneries, imekuwa ni muda mrefu sasa tunakipiga kelele. Viko vyuo vya ngozi lakini watu hao hata wakimaliza mafunzo hawana sehemu za kwenda kujifunza. Mimi niombe Waziri ulichukue hili, Mwanza Tanneries ipo, majengo yapo, mitambo yote ilishaondolewa, hebu mliangalie na hili kama ni kutafuta wawekezaji watafuteni wawekezaji waje haraka tuendelee kunufaika na huyu mnyama anayeitwa ng’ombe na kadhalika kwa ajili ya ngozi hizi ambazo kwa kweli zitaweza kutuletea pato kubwa sana kwenye taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie habari ya biashara ya mabondo; biashara hii ni kubwa sana, na Wachina wamejaa Mwanza wananunua mabondo. Bahati mbaya sana ni biashara ambayo haina bei elekezi. Mheshimiwa Waziri, inawezekana Wizara na Serikali inapoteza fedha nyingi sana. Mchina mabondo yakiwa mengi kabisa; maana hawa samaki Sangara wakati mwingine wanakufa tu na kiferezi huko kwenye maji, mabondo yanongezeka, akija Mchina haulizi bei, matokeo yake anashusha bei inakuwa ya kutupa kwa sababu mabondo yamekuwa mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hii haiwezi kuwa sahihi sana. Ni lazima tufike sehemu tuweke bei elekezi ili huyu anayechuuza na yeye kupata biashara hii asinyanyasike kwa sababu tu Serikali haijawawekea mwongozo lakini inataka kodi ya yale mabondo. Kwa hiyo lazima tuangalie maeneo yote mawili ili tuweze kumsaidia mvuvi, tuweze kumsaidia mtu anayefanya biashara ya mabondo, lakini tumuwekee mkakati huyu mfanyabiashara anayekuja kununua ajue msingi wa Serikali unataka nini kwenye biashara ya mabondo.

Mheshimiwa Spika, liko lingine, hili nafikiri baada ya Wizara kuwasilisha hii bajeti nitamwona Mheshimiwa Waziri nimletee na hawa watu, walinyanyasika sana na mzigo wao mkubwa wamedhulumiwa, lakini kila wakifuatilia baada ya maamuzi ya Mahakama wanachukuliwa hatua, inakuwa kama ni kazi ya uhasama. Sidhani kama ni vyema kulisema hapa, lakini nalisema kama brief, halafu nitamtafuta Waziri na hawa watu ili aweze kuzungumza nao.

Mheshimiwa Spika, lingine, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwenye suala la uvuvi wa samaki, kiukweli wamefanya kazi kubwa. Jambo lililopo sasa la uamuzi wa kutoka kwenye sentimita 50 kwenda 85 kwa kuamua kuiruhusu 85 hata kama itafika sentimita 200, huu ndiyo uamuzi mzuri na nampongeza sana Mheshimiwa Waziri. Tunataka kama hivi jambo limetokea wamechukua hatua wamekaa wamefikiria wakaamua kwa ajili ya maslahi ya watu, hongera sana, samaki huyu mwenye sentimita 85 na kuendelea ndiyo mwenye soko na ndiye anayelipa kuliko Waziri anavyofikiria.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la nyavu, sote tunafahamu kwenye suala la nyavu, nyavu za dagaa pamoja na nyavu za sangara ambazo ni milimita nane mpaka milimita sita. Kwenye nyavu za sangara Waziri ameshafanya utafiti zaidi ya mara mbili na jambo moja kubwa tunaona kwamba nyavu za single, maana kuna double na single, nyavu za single ni ukweli kwamba pamoja na tafiti mbili alizozifanya Waziri, inaonekana bado haziwasaidii wavuvi kufikia malengo waliyoyakusudia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri turudi pale kwenye double wala asikate tama, arudi pale kwenye double ili wavuvi kulingana na mawazo wanayoyatoa kwa sababu ndiyo wako kwenye field, ataona matokeo yake, Serikali itapata fedha, samaki anazozitaka zitapatikana, vipimo vilivyokadiriwa vitapatikana na tutakuwa hatuna tatizo kabisa.

Mheshimiwa Spika, zaidi ya yote nafahamu sasa hivi Mheshimiwa Waziri anafikiria kuwa na pie kati ya sita au saba, hebu nimwombe tusimame kwenye six pie au turudi chini kuliko kwenda kwenye…

SPIKA: Malizia Mheshimiwa Mabula, dakika moja.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, hizi zinaweza zikatusumbua sana kwa sababu mzigo utaenda kwa wavuvi na sio kwa watu wengine.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, nafikiri kwa leo hayo machache yanatosha, naunga mkono hoja kwa asilimia mia na Mungu awabariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi walau ya kuchangia mchana huu ili niweze kusema maneno machache ambayo nadhani yatakuwa na faraja sana kwangu na kwa wananchi wa Jimbo la Nyamagana na Taifa zima kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, kwa haraka naomba nianze kwanza kwa kumpongeza Waziri pamoja na Naibu Waziri na Wizara nzima kwa ujumla kwa namna ya kipekee ambavyo wamekuwa wakifanya kazi kwa ushirikiano na ushirikiano huu ndiyo ambao umetuletea ahueni ya kutatua migogoro mingi sana kwenye nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka kwenye bajeti ya mwaka jana tulilalamika sana juu ya vifa avya utendaji kazi kwenye halmashauri nyingi. Waziri aliahidi na ametekeleza hili kwa vitendo na tumeona vifaa na kwenye halmashauri zingine zimefika.

Mheshimiwa Spika, tulisema; mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PAC, tulilalamika sana juu ya uwepo wa kukosekana kwa Bodi ya NHC, nimshukuru sana Waziri kwa kulifanyia kazi na kuhakikisha Bodi inapatikana na sasa kazi inaweza kufanyika vizuri na hata malalamiko mengine yale yaliyokuwa pembeni yanaweza yakaanza kufutika haraka.

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye suala la urasimishaji makazi. Suala hili ni ukweli kwamba ziko changamoto nyingi sana na wananchi wengi sana kwenye Taifa hili waliokuwa wamepoteza amani leo naamini wanayo amani kubwa. Waliokuwa wamepoteza matumaini leo naamini wamerejesha matumaini na wale waliokuwa wanaenda kuwa maskini wa kutupwa, leo wamerudi kuwa na uhakika wa kuendelea na utajiri wao.

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi nchi hii yalikuwa yameshachukuliwa yamejengwa na wananchi, wananchi wengi wamekaa kwenye maeneo ambayo hayakupaswa tena kuwa ni maeneo ya makazi na hii inatokana na michoro mingi nchini kutokusimamiwa vizuri pale inapokuwa imeshachorwa. Lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na Waziri Lukuvi kwa jambo moja kubwa la kuamua kurasimisha makazi. Leo tunazungumza hapa sisi kama Nyamagana pamoja na jiji la Mwanza kwa ujumla, zaidi ya makazi 12,000 wamepata hati za makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili sio jambo dogo. Nitumie nafasi hii kuwashukuru sana watendaji wa mamlaka na hi ardhi kule Mwanza Jiji pamoja na Manispaa ya Ilemela, kwakweli wamefanya kazi kubwa sana niendelee kuwatia moyo, hakuna kazi kubwa kama kuwatumikia wananchi wanyonge ambao wanahitaji kupewa ahueni kila siku ili waweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala bomoabomoa. Bomoabomoa hii Mheshimiwa Waziri leo tena amesema; mwananchi ambaye yuko kwenye eneo ambalo halihitajiki kuweka barabara, eneo lilotengwa miaka iliyopita kama limetengwa kwa ajili ya ujenzi wa kitu kinachoweza kujengwa eneo jingine tumuache mwananchi huyu asivunjiwe nyumba ili aendelee kuishi na tumrasimishie makazi yake.

Mheshimiwa Spika, zaidi ya yote suala la mpango kabambe. Naenda haraka kwa sababu ya muda. Mheshimiwa Waziri huu mpango kabambe Mwanza umefanya vizuri sana na sisi mwanza kama ulivyosema nah ii ni kazi kubwa inayofanywa na watendaji wa ardhi wa Jiji pamoja na Manispaa ya Ilemela na kile kikosi kazi kilichotengenezwa kwa ajili ya kusimamia mpango kabambe. Yako maeneo Mheshimiwa Waziri, hayana sifa ya kupimwa kwa maana kwamba yanayo sifa lakini yako kwenye maeneo ya vilima. Mheshimiwa Waziri unajua, sisi Mwanza tuna milima mingi na wakazi wengi sana wamejenga kwenye vilima hasa vilima vya kule Isamilo, Mabatini, Igogo lakini hata maeneo ya mbugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jambo pekee Mheshimiwa Waziri, maeneo haya hayawezi kupewa hati za miaka 90 kama wengine lakini umezungumza suala la leseni za makazi. Nikuombe, hii 5,000 5,000 kule Mwanza ni nyingi sana. Wakazi kule milimani wanaweza kutoa fedha hii wakati wowote. Nikuombe uje Mwanza, uzungumze na wananchi wanaoishi kwenye maeneo ya milima uwapatie leseni za makazi ili na wao waweze na uhakika na maeneo yale ili mpango kabambe utakapokuja Mheshimiwa Waziri kusiwe na tatizo tena, mtu awe na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anayekuja kwa ajili ya kutwaa lile eneo ajue anazungumza na nani ambaye atakuwa tayari kumuachia lile eneo kwa ajili ya kuendeleza mpango na wananchi hawana tatizo, wako tayari na wamekuelewa sana. Zaidi ya yote Mheshimiwa Waziri, niseme tena, umeondoa umaskini kwa Watanzania wengi, umeondoa unyonge kwa Watanzania wengi na zaidi ya yote endelea kusaidia maeneo mengi bado yanaweza kutaka kubomolewa kwa namna ambavyo unatuongoza maelekezo haya yaende mpaka kule kwenye Kata, mpaka kule kwenye halmashauri ili tuweze kuwasaidia wananchi hawa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kujenga nyumba ni miaka 10 na mimi nawashangaa ndugu zangu wanaolalamika. Nilikuwa naona hotuba hii lakini kwa sababu Mheshimiwa Spika alishatos mwongozo mzuri na mimi nisirudie kule lakini niseme maeneo yote ambayo kwakweli yanastahili kuacha njia kwa ajili ya kuwasaidia Watanzania, leo ukienda pale kwa Mheshimiwa Kubenea pamoja na kwamba kulikuwa na majonzi lakini leo ni faraja na hata eneo linaongezeka thamani Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, ni lazima tuwe tunafika sehemu nyingine wakati fulani tunaona hili ni sawa lakini tunafahamu maumivu yanaingia kwa kasi na yanatoka polepole sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, nikushukuru sana kwa kazi nzuri mnayoifanya, tunaomba muendelee kutusaidia na kulisaidia Taifa hili ili tuweze kusonga mbele. Ubarikiwe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na Mungu akubariki na jana nimeona umefanya kazi nzuri sana ya kutoa tunzo za Mo Awards kwa wachezaji wa Simba. Ubarikiwe sana, hii ni kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia 100. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi jioni hii ili niweze kuchangia walau maneno machache kuhakikisha kwamba bajeti yetu inakuwa ni bajeti bora kama ambavyo tumeipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nianze kwa kuwapongeza na kumshukuru Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa namna ambavyo wamekuwa wakitenda kazi na wajibu wao sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba moja kwa moja nijikite kwenye suala zima la hali halisi ya viwanda. Tunafahamu kwamba Serikali yetu inayo dhamira njema ya kuhakikisha viwanda vyote vilivyoko nchini vinapata nguvu, vinawezeshwa, lakini viwanda vyote ambavyo vinategemewa kujengwa hapa nchini vijengwe kwa misingi ya kuzalisha lakini kwa misingi ya kutoa ajira na kuifanya nchi yetu kuwa nchi ya viwanda halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwanza tuna viwanda vya samaki karibia saba mpaka nane. Hivi tunavyozungumza leo ni viwanda takribani vitatu au vinne peke yake ndiyo vinafanya kazi na vyenyewe havifanyi kazi kwa ufanisi unaotakiwa. Lipo tatizo moja kubwa, mwanzo baada ya operesheni tunafahamu kabisa Serikali ilikuja na bei elekezi ya samaki kuanzia karibia shilingi 5,500 mpaka shilingi 6,000. Leo kilo moja ya samaki inauzwa shilingi 3,800. Huyu mvuvi ili akavue wale samaki sawasawa na kuwaleta anagharamikia zaidi ya lita moja ya mafuta kama unavyofahamu kwa sasa ni shilingi 2,480 hadi 2,500.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema kuwa Serikali imeachaniza hii sekta ya viwanda vya samaki, imewaacha wenyewe wafanyabiashara na wenye viwanda wahangaike kutafuta masoko, wahangaike kutafuta bei ambazo zinaweza kuwasaidia kwenye mafuta, wahangaike wenyewe kuona namna ambavyo wanaweza kuendesha viwanda hivi. Kiwanda kimoja peke yake kilichokuwa na uwezo wa kuajiri wafanyakazi zaidi ya 700 leo kinaajiri wafanyakazi 50 mpaka 90 kwa shift moja, kilikuwa na uwezo wa kukata tani 70, leo kinakata tani 15 peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali haitawekeza jicho huku na nimuombe sana Mheshimiwa Waziri hasa Waziri wa Uvuvi warudi nyuma waangalie kushiriki na wavuvi hao wote ili waweze kushughulikia suala hili la viwanda vya samaki, vinginevyo vitakufa, tutaendelea kupoteza ajira na wafanyabiashara ndogo ndogo sio kwamba wanapenda kuweo wengi, wanakuja kwa sababu hakuna kazi za kufanya ndiyo maana wanatafuta mitaji ya shilingi 200,000 waingie sokoni ili waweze walau kuuza bidhaa yoyote ile wajikimu na maisha yao.

Kwa hiyo, niombe sana bidhaa hii jhasa bei ya samaki lazima irudi kuwa elekezi ili wavuvi nao wanakovua kule waone umuhimu na faida ya kwenda kukesha kwenye maji na kurudi nchi kavu kufanya biashara na viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nilitaka kuzungumzia Wakala wa Barabara (TARURA). Nimekuwa nikisema siku zote kwamba mimi ni muumini mzuri wa TARURA, kwenye bajeti iliyopita tumeongeza fedha kwa ajili ya bajeti ya TARURA, inakadirika shilingi bilioni 30 baadae tena ikaongezwa karibia shilingi bilioni 60 hivi na mimi nataka kusema jambo moja; TARURA kama tutaijali, kama tutaichukulia kama chombo ambacho tumekitengeneza kwa ajili ya kuja kutoa suluhisho kinaweza kufanya kazi nzuri sana. Suluhisho tunalolizungumza hapa kwenye chombo hiki ni lazima fedha zote zilizotengwa na fedha zilizoongezwa kwenye bajeti zielekezwe TARURA ili waweze kutoa mgawanyo ambao ni sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukichukua kwa mfano Wilaya mbalimbali zilizoko kwenye Jiji la Dar es Salaam na Wilaya zilizoko kwenye Majiji mengine kama Mwanza, leo ukichukua Kinondoni na Nyamagana ni kama vile tunalingana lakini ukija kwenye mgao Nyamagana inapata kidogo, Kinondoni inapata zaidi na hii sio sawa kwa sababu hata miji yote iliyoko pembezoni inahitaji kufunguliwa mtandao wa barabara ili tuweze kwenda sawa na mazingira tunayoyapigania sasa. Vinginevyo tutabaki kupiga kelele humu, fedha ziongezwe halafu fedha zisipokwenda hata utekelezaji wa miradi yenyewe hautafanana na kile ambacho tunakipigania kelele na tunachokiombea kila siku hapa.

Kwa hiyo mimi niombe sana, narudia; TARURA ni chombo muhimu na TARURA wameanza kuonesha njia. Kama watapewa fedha kama ambavyo tumekubaliana kwenye Bunge hili wakati wa bajeti iliyopita ya kisekta sina shaka TARURA wanaweza kufanya kazi yao vizuri na mgawanyo narudia tena, uwe sawa kulingana na mahitaji ya kwenye kila mji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili liende sambamba na ahadi zilizokuwa zimetolewa na Mheshimiwa Rais hasa kwenye maeneo haya am bayo sasa yamekabidhiwa TARURA, mimi nina barabara karibia tatu za ahadi ya Mheshimiwa Rais, niombe sana barabara ya kutoka SAUT – Luchelele; Igoma – Kishiri kutokea Buhongwa; hizi ni ahadi za Mheshimiwa Rais na barabara hizi zimerejeshwa TARURA ni lazima sasa TARURA waje na mpango wa kutuambia barabara hizi zinajengwaje na Serikali ipeleke fedha hizi ili barabara hizi zijengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la umeme; tunafahamu REA haitoi huduma wala ujenzi wa miradi ya umeme kwenye majiji kwa maana majiji haya yote yana mitaa na hayana vijiji, lakini mimi nimuombe sana Waziri wa Fedha pamoja na Waziri wa Nishati wafikirie jambo hili, tunachukua umeme tunapeleka vijijini, hatukatai, ndiyo mfumo. Leo wamekuja na umeme wa mradi wa peri-urban, huu mradi wa peri-urban kama hautakuja kutekelezwa sawasawa, miji yetu itabaki kuwa na giza ilhali watu wamejitoa na wamejenga majumba kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Kwa hiyo mimi niombe mradi wa peri-urban utakapoanza uelekezwe kwenye maeneo ambayo ni very strategic na hii ni biashara, TANESCO wanafanya biashara hapa, wanaingiza fedha. Sioni sababu unapeleka transfoma mbali kwa miaka miwili wameunganisha watu wanne badala yake tunapoteza fedha. Walete hizi transfoma mjini watu wamejenga zaidi ya kaya 15,000/20,000 kwenye kila kata ili tuweze kupata suluhisho la mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho tumejikita kwenye miradi mikubwa sana na sasahivi Serikali inafikiria kwenda kujenga mradi mkubwa wa kuhifadhi mafuta kwa pamoja. Tunakwenda tunafikiria tutatumia zaidi ya dola bilioni 22 lakini sisi tuna wadau, tuna PUMA na TIPER, hawa sisi tuna hisa asilimia 50 kwa kila kampuni. Lakini kama ndiyo msimamo wa Serikali, hebu tusubiri kwanza tuimarishe hii miradi mikubwa tulinayo, hiyo dola milioni 22 ukiipeleka kwenye Stiegler’s Gorge, ukiipeleka kwenye standard gauge tutakwenda mbali zaidi kuliko kufikiri kujenga matenki ya mafuta leo na huku ni ku-frustrate wadau tulionao.

Kwa nini tusikae na hawa wadau? Maana shida ya Tanzania sio kuwa na reserve ya mafuta, shida ya Tanzania tulikuwa na uhaba mafuta yanapotoka yanaletwa na nani. Sasa tumeshamaliza mfumo huo, mafuta yanaagizwa kwa pamoja, yanakuja kwa pamoja. Bado iko tatizo, hata leo ukienda bandarini pale tunajenga flow meter mpya. Hivi ile flow meter ya zamani kule Mji Mwema ina matatizo gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumechunguza matatizo yake? Tumebaini matatizo yake? Haitoshi, tunafanya ujenzi mpya, tume-engage mkandarasi mshauri, hatumtumii, tunamuacha kama alivyo, leo tunafikiria kuwekeza mradi mwingine tuwatengenezee watu kichaka kipya na hii ndiyo maana tunaambiwa sisi tunaotunga sera na kuzisimamia tuanzidiwa sana maarifa na watu wanaofanya baishara hizi kule nje na hii sio sawa. Ni lazima maarifa ya watunga sera na wanaozisimamia sera yawe na weledi mkubwa kuliko hawa walioko nje ili tuweze kwenda sambamba na kazi ambayo tunaifikiria na kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema tunatamani sana miradi hii mikubwa ikamilike kwa wakati, Stiegler’s Gorge, standard gauge ikifika Mwanza wananchi wa Mwanza watakuwa na ahueni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naomba kuunga hoja mkono asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kukushukuru wewe, kulishukuru Bunge lako, na kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa namna ambavyo ameendelea kutupa nafasi ya kuwepo hapa ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze kwa uamuzi mzuri wa kuamua kuleta maazimio haya mawili ndani ya Bunge kwa sababu kubwa mbili. Moja ni kumuenzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambaye alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kumpongeza mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye leo ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna maneno mazuri sana ya kusema leo, lakini ukweli ni kwamba inawezekana kulingana na vitabu vitakatifu yako mambo yameandikwa kwenye vitabu hivi vitakatifu, na sisi kama wanadamu tunaoishi tusioijua leo wala kesho na mipango yote kama ambavyo Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye leo jina lake limeletwa mbele yetu na ametuambia mambo yote mazuri yanatoka kwa Mungu, hatuna shaka ya kwamba kipindi alichohudumu Dkt. John Pombe Magufuli ndio wakati wake aliopewa na Bwana kutenda yale aliyoyatenda na sisi kama Watanzania tuyaone na ikiwezekana tufate dira hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesikia tamko hapa, Azimio la Kumpongeza Mheshimiwa Rais, mama yetu Samia. Hakika ni kwamba huwezi kutenganisha shughuli iliyofanywa na Dkt. John Pombe Magufuli na mama yetu Samia Suluhu ambaye alikuwa Makamu wa Rais. (Makofi)

Kwa msingi huo, hatuna shaka mama aliyepokea kijiti hiki amekipokea kutoka kwa mtu sahihi, na kwa sababu ya maandiko amekipokea wakati sahihi na hatuna shaka atalivusha taifa hili kama ambavyo wengi tunayo matumaini makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sisi kama Watanzania na sisi kama Wabunge tunafahamu lindi kubwa ambalo tunapita sasa. Lakini mimi niombe kutumia nafasi hii, nafasi ambayo leo tumepata mabadiliko ya uongozi bila kutegemea, ni wakati ambao sisi kama taifa na watu tuliopewa dhamana, ni wakati sasa wa kutenda sambamba na yale tunayoamini kwamba yatakwenda kuwasaidia Watanzania walio wengi na maskini.

Tumejionea mfano amesema hata Mheshimiwa Dkt. Mpango hapa asubuhi namna ambavyo umati tuliouona kwenye kila mkoa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alikopita, ni ishara ya kwamba watu wanatamani kuona changamoto zao zinasemewa na kutatuliwa kwa kina na kwa vitendo.

Hatuna shaka mama ambaye naamanini sana. Na tumpe heshima hii ya kumuita mama, tusiseme tu mwanamke kwa sababu tunaamini ni wakati wa wanawake lakini tukimpa mama tunakuwa tunamtengenezea heshima na uzito mama huyu ambaye kwa mara ya kwanza katika taifa letu amepata nafasi hii na ninaamini anakwenda kutengeneza historia ambayo itajengwa na itakaa kwenye vizazi na vizazi kwa sababu inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikia siku moja akihojiwa na TBC, ni namna gani anawaza na kufikiria kama ipo siku nchi hii itapata Rais mwanamke. Mama huyu kwa hekima akasema kama imetokea leo kwa mara ya kwanza Makamu wa Rais ni mwanamke, kwa nini huko mbele isiwezekane? Jambo lolote chini ya jua linawezekana kama tu Mungu amekupangia safari hiyo.

Kwa hiyo inawezekana hakujifikiria yeye akafikiria watu wengine kwenye vizazi vinavyokuja; lakini hakika kumbe Mungu alimpangia yeye na hakika amempa. Tumuombee dua, tumuombee mapenzi makubwa, lakini kikubwa zaidi tuendelee kumuombea hekima, busara na uchapaji kazi ambao utatupa dira na kutuonesha Watanzania. Safari iliyoanzishwa na Dkt. John Magufuli ndiyo kwanza sasa imeanza kwa sababu imepokelewa na mama, na wote tunaamini mama akiachiwa familia watoto hawawezi kufa njaa, na vivyo hivyo, Tanzania haiwezi kubaki kama ilivyokuwa, tutakwenda kwenye wakati ambao tutavuka salama, na tena salama kuliko wakati wowote. Bwana ambariki sana Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan na aendelee kumpa mapumziko mema huko aliko Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono maazimio yote mawili. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii, nikiwa naenda kufunga dimba kabisa kwa siku ya leo, nikushukuru sana. Nami niungane na wenzangu wote kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri na timu yake nzima ya TAMISEMI, Katibu Mkuu na wasaidizi wake kwa kuendelea kuaminiwa na Serikali ili waweze kuitumikia na kututendea kazi ambayo Serikali inakusudia kuifanya kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapindunzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianzie pale ambapo Mheshimiwa Mavunde ameishia. Ukweli ni kwamba majiji yetu na Manispaa, Miji pamoja na Halmashauri ambazo zinakua, zimenufaika sana na mradi wa TSCP na sina shaka, kwa rekodi peke yake kutoka mwaka 2010 mpaka mwaka 2020 kwa hii miaka 10 peke yake majiji yapatayo sita, Manispaa karibia nane pamoja na miji zaidi ya 16 imefaidika sana kwa miradi ya TSCP.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukienda hata Babati, Manispaa ya Ilemela, Mwanza, Tanga, Mbeya kule kwako zaidi ya kilometa 438 zimejengwa. Sasa naiomba sana Serikali, Mheshimiwa Waziri atakapokuja, kama Mheshimiwa Anthony Mavunde alivyosema, tuone namna gani mradi wa TACTIC ambao tayari wataalam kutoka World Bank na wataalam wa ndani, wameshatembelea Halmashauri zetu na kujiridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, inasemekana yapo mambo machache tu yamekwama huko kwenye Wizara, hebu tuyatazame tuone namna ya kuruhusu mradi huu uanze mara moja tuweze kuona tija ambayo tumeipata kutoka miradi ya TSCP na hatimaye tuone mafanikio na turahisishe, tupunguze mzigo kwa TARURA ambapo wote humu ndani tunalalamika kwamba fedha hazitoshi. Mradi huu tuna uhakika utahudumia zaidi ya Halmashauri 45 ukilinganisha na Halmashauri 18 na 9, jumla 27 peke yake kwa kipindi kilichokwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema nianze na hilo kwa sababu ni jambo muhimu. Naamini ukienda kule Mbeya, Tanga, Mwanza na hapa Dodoma na maeneo mengine ya Arusha, bado zipo barabara ambazo zinaunganisha miji hii na zitaleta tija sana katika mchango wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jiji la Mwanza peke yake tunategemea kuwa na barabara zisizopungua Kilometa 27 hadi 33. Barabara ya kutoka Buhongwa kwenda Igoma, barabara ya kutoka Sauti kwenda Luchelele, barabara ya kutoka Buhongwa kwenda Bulale inayokwenda kuungana na daraja la Masongwe kwenye Halmashauri nyingine ya Misungwi. Haya yote ni mafanikio ambayo yanaweza kuchagizwa sana na barabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni juu ya masuala mazima ya ardhi na upimaji. Utakubaliana nami kwamba jukumu la upimaji na Sheria ya Ardhi Na. 8 imezipa mamlaka zetu haki ya kupima, kumilikisha pamoja na kupanga. Sasa nimejaribu kuangalia kwenye kitabu, sioni maeneo ambayo Wizara imekumbuka kupeleka fedha kwenye Halmashauri zetu ili jukumu la kupima, kupanga na kumilikisha liweze kufanyika huko kwenye Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miji yetu bado ina changamoto kubwa. Kama Wizara inafanya jukumu lake la kupeleka watumishi na kuwalipa mishahara kupitia Wizara ya Ardhi, lakini jukumu la kwetu kama Wizara ya TAMISEMI ni kuhakikisha Halmashauri inaendelea kupima, kupanga na kumilikishwa ili tutoke hapa kwenye maeneo ambapo tupo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine la muhimu kwenye Sekta ya Afya, upo mpango ambao ulipokelewa hapa na Wakurugenzi pamoja na watendaji kwenye Halmashauri. Maelekezo ya namna gani kila Halmashauri kulingana na mapato yake, kwa mfano, Jiji la Mwanza peke yake tumepangiwa kujenga vituo vya Afya vitatu, tujenge madarasa 100. Sasa nadhani hapa bado kuna changamoto tuiangalie vizuri. Mipango iliyopangwa kwenye Halmashauri na kuletwa bajeti kwetu, maana yake ni kwamba haitatekelezeka kama Halmashauri zitapokea maelekezo haya ambayo zinayo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi leo hatuhitaji madarasa, maana yake tukisema madarasa, tunataka tukaongeze darasa kwenye kila shule. Sisi tunataka shule mpya. Tunazo shule 28; kila shule moja kati ya shule hizi, shule 27 kila shule ina watoto wasiopungua 2,400 sawa na shule nne. Kwa hiyo, tunadhani sisi leo tukiamua tunataka tujenge shule mpya zitakazowasaidia watoto hawa kukaa kwenye mazingira bora, salama na rafiki na yanayoweza kufundishika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninafahamu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naona umewasha kengele hapa, muda wenyewe umebana, lakini nakushukuru sana. Niseme tu kwamba tunahitaji mipango iliyopangwa na Halmashauri iweze kupokelewa na kuruhusiwa kufanya kazi ili iweze kuleta matunda na faida kwa wananchi kuliko maelekezo haya.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, Mungu akubariki. Ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, na nitumie nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi walao niseme kidogo juu ya Wizara ya Maji kwasababu, ninaamini ili wananchi wetu waweze kufanikiwa kwenye mahitaji yao mengi wanahitaji maji safi salama na maji kwa wingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba, Wizara ya Maji imefanya kazi kubwa sana, sana kabisa, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima pamoja na Wizara kwa Ujumla, chini ya Katibu Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu muda wetu ni mchache sana na kwa hizi dakika tano niseme walao mambo matatu; la kwanza Mheshimiwa Kiswaga amezungumza ni vyema sana Wizara ikaendelea kutusaidia katika wakandarasi ambao tumeshawapata kwenye miradi yetu. Kwa mfano mradi wa chanzo kipya cha maji pale Mwanza, mradi ambao ni mradi bora na utakaosaidia sana Jiji la Mwanza kupata maji. Mkandarasi inawezekana akakwama kwa sababu hajapata msamaha wa vifaa vinavyotoka nje ambako alikuwa anafanya kazi nyingine. Ninaamini mkandarasi akipata vifaa hivi kwa wakati tutakuwa tumepiga hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, ninaendelea sana kuishukuru Wizara kwasababu ya kazi kubwa iliyofanya. Tunao mradi unaoendelea huu wa chanzo kipya cha maji na usambazaji wa bomba kutoka kule Lwanima kwenda Butimba kupitia Sawa kwenda Kanindo kwenda Igoma kwenda Kishiri utakaosaidia mpaka watu wa Buhongwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, liko tatizo na inawezekana sio la Wizara likawa linaunganisha na Wizara ya Fedha. Tunapompa mkandarasi kazi kuna kitu kinaitwa GN – Government Note; Government Note inatoka ya mwaka mmoja-mmoja. Tunapotoa Government Note ya mwaka mmoja wakati mkandarasi ana mkataba wa miaka miwili au miaka miwili na nusu tafsiri yake ni kwamba, atakapokuwa ameanza ujenzi wa mradi ile GN unakuta imeshaisha muda wake analazimika kusubiri tena miezi mitatu mpaka miezi sita. Hii inafanya tunachelewesha sana wakandarasi tuliowapa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ili twende vizuri ninadhani Wizara ya Fedha ikubaliane na Serikali na Wizara ya Maji inapotoa GN itoe GN ya uhai wa mkataba, lakini ikiwa imeongeza miezi 12 itakayoisadia Wizara kumsimamia mkandarasi vizuri na kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na la tatu na la mwisho, ninafahamu Mji wetu wa Mwanza unakuwa kwa kasi. Mpaka sasa tunacho chanzo cha maji kinachozalisha zaidi ya lita milioni 90. Mahitaji ya Jiji la Mwanza, Nyamagana, Ilemela, Magu mpaka Misungwi ni zaidi ya lita milioni 160 na hizi milioni 90 tunazitumia sote kwenye hizi wilaya takribani tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe. Tunao mradi wa Mwanza South tunautegemea sana na sasa tuko kwenye hatua za mwisho. Wataalamu wanasema wanasubiri no objection, Serikali iongeze nguvu ili tupate huu mradi ambao sina shaka utasaidia sana kwenye maeneo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatarajia tukipata fedha hizi tutajenga tenki la lita milioni sita kule Nyamazobe litakalowasaidia sana watu wa Malimbe, watu wa Luchelele, pamoja na Chuo Kikuu cha SAUT ambacho kiko Nayamagana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hiyo tu maeneo yote ya kwenda Igoma, maeneo yote ya Buhongwa. Maji haya yatakwenda mpaka Kisesa kule kwa Mheshimiwa Kiswaga, yatakwenda mpaka kule kwa Mheshimiwa Pastory Mnyeti kule Usagara na kwa kufanya hivi yatakwenda mpaka Ilemela. Hapo tutakuwa tumekidhi walao mahitaji kwa asilimia 98 ya watu wa Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi ya yote nikupongeze sana Mheshimiwa Aweso na msaidizi wako, ndugu katibu na timu nzima mnafanya kazi nzuri, mnakwenda kila mahali na kwa kweli mnaitembelea miradi yenu. Mungu awabariki sana na sina shaka kazi tuliyobakisha ni kusema ndio na shilingi yako mzee upambane kuhakikisha maji yanatufikia. Bwana awabariki sana, ahsanteni. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa sababu ya muda na mimi nianze kwa kuishukuru sana Wizara ya Nishati, nimshukuru Waziri, Naibu Waziri na Wakurugenzi wake wote ambao wanashughulika kuhakikisha Watanzania wanapata umeme wa kutosha. Ukweli ni kwamba TANESCO pamoja na Taasisi hii wamefanya kazi kubwa sana. Ukikumbuka toka mpango huu uanze mwaka 2014 Awamu ya Tano ilipoingia, Awamu ya Sita leo tunaendelea nayo kumekuwa na jitihada kubwa sana na wananchi wetu mahitaji yao mengi ukitoa maji, umeme na barabara na afya jambo kubwa sana wanatutazama namna gani tunapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda niongelee mambo mawili tu, suala la usambazaji wa umeme, ukweli ni kwamba kazi kubwa sana imefanywa. Ukitazama scope ya kazi ambazo wanapewa wakandarasi zinakuwa ni ndogo sana kulingana na mahitaji ya maeneo husika. Kwa mfano, ukiangalia Jimbo la Nyamagana tumebahatika kupata miradi ya REA na sababu na sifa tulikuwa nazo kwamba tunayo maeneo kwenye mitaa yana sifa sawa na vijiji.

Mheshimiwa Spika, maeneo haya yalistahili na unapopata kata kwa mfano ina mitaa mitano ambayo ipo eneo moja ina zaidi ya kilometa 100 kwa mfano au 80 inapata LV kilometa zisizozidi 20 peke yake ni kuendelea kuongeza lawama kwenye Serikali. Mheshimiwa Waziri nikuombe hata tunapofanya miradi ya densification tujitahidi sana kwenda mbali ya pale tulipoanza, kama tulitoa LV kilometa 12 tusirejee tena kutoa chini ya 12 twende mbele zaidi ikiwezekana 20 na kadhalika. Sisi kwa Nyamagana nataka nikuhakikishie kwamba Mheshimiwa Waziri amefanya kazi kubwa sana na hii kazi aliyofanya imewasaidia wananchi wengi wa Jimbo la Nyamagana kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee miradi ya Peri Urban itakuwa mkombozi na kulisaidia sana Shirika la TANESCO. Kwa nini Peri Urban ifanyike kwa kasi na jana nimeona Waziri ametoa orodha ya wakandarasi wa REA naomba na orodha ya wakandarasi wa Peri Urban tuipate ili tujue scope yetu imekaaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwanza peke yake ukichukua Ilemela na Nyamagana Mheshimiwa Waziri nataka nikuhakikishie ukipeleka leo umeme wa Peri Urban malipo ya watu wake na unit wanazotumia kwa siku mpaka mwezi siyo sawa na maeneo mengine unaweza kuyalingalisha. Hatukatai umeme usiende kila sehemu lakini Waziri atakubaliana nami kuna sehemu unafunga transformer leo ya kuhudumia watu 50 miaka minne umewaunganisha watu wasiozidi kumi peke yake, hii ni hasara kwa TANESCO na lazima muangalie namna bora ya kuwasaidia mnapoweka miradi ya uzalishaji kwa haraka inasaidia sana maeneo yetu mengi.

Mheshimiwa Spika, ukienda Kata za Igoma, Kishiri, Lwanima, Buhongwa, Nyangu, Nyakabwe Mheshimiwa Waziri alitusaidia alipokua na Waziri Mkuu, lakini ukweli ni kwamba tatizo bado ni kubwa na eneo lililopata ni karibia kilometa 12 peke yake eneo lililowazi zaidi ya kilometa 32. Bado ni changamoto na wananchi wanalalamika wanaona kama tumewatenga na tumewabagua lakini ukweli ni kwamba mahitaji ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafahamu hata ukienda Ilemela pale kwa mama yangu Mheshimiwa Angeline kule kwenye Kisiwa cha Bezi bado kuna changamoto kubwa hakuna umeme na uliopo ule wa Jumeme ni kama matatizo yaliyopo hapa kwa ndugu yangu Mheshimiwa Shigongo. Mheshimiwa Waziri umefanya kazi nzuri na kubwa sukuma hapa ulipobakisha, umaligije ikazi ishile na tulole yingi lulu ihaha, mambo yanakuwa yameenda hivyo vizuri au siyo bwana, lakini ukweli ni kwamba kazi kubwa mnaifanya. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mabula ng’welage geke. (Makofi/ Kicheko)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, ee welelagwa gete, welelagwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwenye hii miji tunayoitaja hata hasa kwenye majiji haya makubwa ni hizi ni fedha tumeziacha. Ukienda hata kwa Naibu Spika kule kwenye Kata za Iziwa, Itengano, Iduda hata Itende na kwenyewe ukifunga umeme wa Peri Urban una uwezo wa kuingiza hela nyingi sana Mheshimiwa Waziri na ikasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa kwa sababu ya muda kumekuwa na mjadala mkubwa sana hapa ambao unaendelea…

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa hiyo inatoka wapi endelea na taarifa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nataka kumwambia mchangiaji Mheshimiwa Mabula kwamba hata maeneo ya Kibaigwa, Kongwa na Sengerema Mjini yote yanahitaji umeme. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Hata kule Ilemela kwa Mheshimiwa Angeline Mabula pia, endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataja miradi ya Peri Urban ambayo watu wa majiji tumeomba ili ije kutusaidia kupunguza mzigo mzito. Mwananchi wa kawaida kabisa anayeishi kwenye majiji ili aunganishiwe umeme anahitaji shilingi 512,000 au shilingi 321,000 ili aweze kufikishiwa umeme kwenye eneo lake. Siyo wote waliopo mjini wana uwezo wa kumudu gharama hiyo ndiyo maana tunaomba watu wa Peri Urban. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kumekuwa na mjadala mrefu sana hapa siku mbili hizi zilizopita na uliuweka vizuri juu ya TBS kupewa zoezi la kuweka vinasaba kwenye mafuta. Nafahamu jana umetoa maelekezo mazuri sana na naomba wakati wanaandaa sheria tufikirie nje ya box, pale bandarini kuna watu wanaitwa Wakala wa Vipimo na Mizani wajibu na shughuli yao kila meli inapotoka na kuingia wanakwenda kupima idadi ya mafuta yaliyokuja, ikifika nje wanakwenda kupima.

Tunapozungumzia kupokea lita karibia laki tano na hao wote ni taasisi zilizoko chini ya Serikali kwa nini tusifikirie vizuri zaidi na Mheshimiwa Waziri hili wakalichakate, tunaweza kuwapa watu wa Wakala wa Vipimo na Mizani, watu wa TBS wakabaki na jukumu lao la kuhakiki ubora wa mali ambayo inaingia nchini kwetu, kwa sababu wamekuwa accredited na dunia wamejulikana na wanatambulika kwa kazi nzuri. Kwa hivyo, nataka niliache kwako, sheria zinapokuja tuzitafakari na tuone namna ya kuziweka vizuri ili tujue sehemu ya kutokea. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja asilimia mia. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia kwa hizi dakika tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na nikupongeze wewe lakini nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Ofisi ya Msajili ya Hazina ambao sisi kama wajumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma tunafanya nao kazi kwa ukaribu sana na hata uzuri ripoti yako unayoiona na uliyoisikia leo ni kwa sababu ya wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie pale ambapo ameishia Mheshimiwa Malima jambo kubwa sana ambalo Serikali inabidi ilifanyie kazi kwa umakini mkubwa ni namna ya kuangalia mashirika haya ambayo tumeyapa nafasi ya kufanya kazi na usimamizi wake kwa namna moja au nyingine tunakuwa na miradi isiyokamilika kwa wakati na kwa mfano mzuri sana ni miradi ambayo iko kwenye shirika la nyumba la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna miradi imeanza muda mrefu lakini iko miradi ambayo imesha-takeoff sasa inakwenda vizuri. Lakini ni kwa nini miradi ambayo bado haijaanza kuchukuliwa hatua mpaka leo takriban miaka 10 haitakiwi kuanzishwa na kuendelezwa mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna miradi ya mfano pale Kawe wanaoishi Dar es Salaam watakuwa wanaijua 711 Kawe na ile Golden Premier Licence Kawe. Hapa kuna mbia lakini huyu mbia kila siku anaingilia hapa anatokea hapa niombe sana Serikali iingilie kati fedha zilizowekwa pale ni fedha za walipa kodi na kama tutaacha hivi tutakuwa tumetupa fedha na hatutakuwa hatuwasaidii watu wa National Housing. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini fedha zinazokuja wakati wa gawio ni moja ya chanzo kizuri sana cha mapato kama taasisi hizi zitafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni kuhusu kiwanda cha viuadudu kama tulivyoambiwa hapa na wenzangu waliopita kiwanda hiki ni mali ya Serikali kupitia NDC kwa asilimia 100. Serikali yetu inapata fedha nyingi sana kwenye mfuko kutoka mataifa na taasisi mbalimbali kwa ajili ya kushughulikia malaria asilimia 98 fedha hizi zinashughulikia ugonjwa wa malaria na sisi tumepata bahati ya kuwa na kiwanda hapa ndani bahati mbaya sana asilimia hizi 98 ya fedha kutoka Global Fund hatuwezi kuzitumia kununua dawa kwenye kiwanda chetu cha viuadudu kwa sababu dawa hizi zinazozalishwa hazijaidhinishwa na ithibati ya WHO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tuna dhamira ya dhati ya kupambana na ugonjwa wa malaria ni lazima tufike sehemu tukubali NDC, Serikali pamoja na hao ambao ni radio farm kutoka Cuba ambao ndiyo wenye hati miliki ya hivi viuadudu wakikaa pamoja shida ya hawa ni shilingi 6% itakayowafanya wao wawasaidie kwenye kiwanda hiki kupeleka WBHO waidhinishe ili dawa hizi zitakazokuwa zinatumika zikubalike kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo pale Uganda wameanzisha ujenzi wa kiwanda cha viuadudu kama hiki tulichonacho sisi hapa NDC. Hebu niambie kikikamilika dawa hizi tutauza wapi? Tutabaki kuhangaika na halmashauri zetu ambazo tumeshatoa maelekezo lukuki lakini hayazingatiwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana na niiombe sana Serikali hivi viwanda tunavyovianzisha kwa nia njema kama hatutakuwa na mpango mahususi wa kuwekeza nguvu na usimamizi mzuri nimesema hapa TR anafanya kazi nzuri sana lakini wakati mwingine kwa namna moja au nyingine anaweza akazidiwa asifikie malengo yake. Kwa sababu kama walivyosema akipia huku watu wanatokea huku ni kitu gani kinachoshindikana kiwanda hiki ithibati hii iende WHO ithibitishwe na dawa hizi katika asilimia 98 ya dawa tunazopata kutoka kwenye Global Fund zikija hapa tutakuwa tumevuka lengo la tumeokoa watanzania wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kukushukuru sana lakini kumshukuru sana Mungu kwa kuendelea kutupa afya njema. Bunge lako hii ni awamu nyingine ya bajeti na nitumie nafasi hii kama wenzangu waliopita walivyokwishasema, Wizara hii iko chini ya Mheshimiwa Rais tumpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu ya kazi kubwa sana inayofanywa na wasaidizi wake. Nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake, lakini Katibu Mkuu pamoja na wasaidizi wake wote kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bunge lako kupitia Wizara hii kama itafanya kazi yake vizuri kwa namna inavyokwenda nina hakika hakuna Mbunge ndani ya Bunge hili atashindwa kurejea hapa kwa sababu hii ndiyo Wizara mama ambayo sote tunaitegemea. Kwa leo naomba nigusie maeneo mawili au matatu.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni eneo la TARURA. Nchi yetu ina barabara nyingi sana ambazo hazijajengwa kwa kiwango kinachostahili. TARURA wamebainisha zaidi ya kilomita 1,044,000 za kiwango cha vumbi ambazo zinatakiwa zijengwe kwa lami. Bajeti tuliyoiona safari hii tunashukuru kwamba imeongezeka kufikia angalau bilioni 800.

Mheshimiwa Spika, lakini ukienda Nyamagana peke yake tuna kilomita zaidi ya 944 ambazo hazijajengwa kwa kiwango cha lami na ni barabara mbaya kabisa. Sasa nadhani umefika wakati kwa Serikali iangalie vizuri Wizara hii ya TAMISEMI na taasisi hii ya TARURA kuhakikisha angalau tunakuwa na mpango wa miaka minne kuongeza fedha angalau zifikie angalau trilioni 1.3 mpaka trilioni 1.4. Kwa kufanya hivyo, ukitazama bajeti ya mwaka huu tumekusudia kujenga kilomita 411 peke yake za lami, lakini kuna miji ina zaidi ya kilomita hizo na mimi nishukuru sana kwa mpango wa TACTIC.

Mheshimiwa Spika, mpango wa TACTIC nafahamu uko kwenye Jiji lako la Mbeya lakini nafahamu uko kwenye Majiji ya Dodoma na maeneo mengine. Mradi huu ni sawa na mradi uliomalizika wa TSP ambao kiukweli umetuachia matokeo makubwa sana na nautarajia sana mradi huu, Mheshimiwa Waziri amesema utaanza mwezi wa Saba baada ya bajeti, nami ninayo barabara ambayo itanufaika na mradi huu, barabara ya kutoka Buhongwa kwenda Rwanima-Kishiri kupita Fumagila mpaka Igoma, lakini barabara hii ni sambamba na ujenzi wa soko la mazao ya majini na nchi kavu.

Mheshimiwa Spika, sasa hii ndiyo miradi ambayo inaweza ikatusaidia, kwanza kupunguza adha na kero kwa wananchi wetu kwa sababu Serikali inafanya mambo mengi mazuri, lakini kama hatutakuwa na barabara bora zenye sifa yote itakuwa ni kazi bure na huko ndiko wananchi wanakopata ghadhabu nyingi. Kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na niishukuru sana Wizara yake na wasaidizi wake kwa kuliona hili na kusukuma fedha na makubaliano ya TACTIC yamefikia mwisho ili tuweze kuona sasa matokeo ya miradi hii.

Mheshimiwa Spika, siyo hilo peke yake, nigusie jingine kwenye sekta ya afya. Tumejenga vituo vya afya vingi sana, tumejenga zahanati nyingi sana kabisa na rekodi ukianzia mwaka 2017 awamu ya kwanza ilijenga vituo 44 ambavyo tunashukuru sana kwa sababu vyote vilipata vifaa tiba. Awamu ya Pili karibu 80%, hivi lakini awamu ya tatu na kuendelea vituo vingi sana havijapata vifaa tiba na kupelekea halmashauri zetu kulazimika kutafuta fedha kwa wadau na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia Jiji la Mwanza peke yake Nyamagana na niombe sana Wizara ukienda Igoma toka kimekamilika leo ukienda hakina vifaa vya msingi vinavyoweza kutoa huduma, ukienda Fumagila na kule Bulale, sasa haya ni maeneo ambayo tunadhani kwa mpango huu ambao Wizara imekuja nao leo.

Nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri wamefikiria vizuri kwa fedha walizozitenga kwa kuongeza kwenye vifaa tiba tufike wakati ikiwezekana bajeti ya ujenzi ipungue, irudi nusu ya tulipo sasa ili fedha nyingi tuielekeze kwenye vifaa.

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu, nitoe mfano, mtu kwa mfano unaenda kwenye kituo kilichoko jirani yako karibu kilometa tano, unafika unaambiwa hatuwezi kukufanyia vipimo uende hospitali ya wilaya, unalazimika kutembea zaidi ya kilomita zingine saba, sasa kuna faida gani ya kuendelea kujenga wakati vituo vingi tulivyovijenga, zahanati na vituo vya afya havina vifaa tiba. Maana yake hapa ni kwamba hatujawasaidia wananchi. Nilikuwa naongea na Daktari mmoja anasema kwa mfano ukiwa na kituo halafu hauna tu peke yake ile mashine ya ultra sound, tunataka kupunguza vifo vya mama na mtoto, kama hatuna kifaa hiki hatuna state ya wazazi kuja kujifungua, hatuna vitanda vya akinamama kujifungulia, bado itakuwa ni kazi bure hatutapambana na wimbi la vifo vya mama na mtoto.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niishukuru sana Wizara kwa kuja na mpango huu wa kuendelea kupunguza fedha kwenye ujenzi na kuongeza fedha nyingi zaidi kwenye kupeleka vifaa ili kila mtu na siyo Nyamagana peke yake, ukienda kule Mbeya kwa mfano kwenye hospitali yako ya Igawilo ambayo imepandishwa hadhi kwenda kwenye hospitali kutoka hospitali ya kawaida kama ilivyokuwa, ina majengo mazuri lakini haina vifaa sasa hivi. Ukienda Iyumbu vile vile kituo cha afya kizuri, lakini hakuna vifaa. Kwa hiyo haya maeneo yote haya ni lazima tuwekeze nguvu ukienda Magu kwa Kiswaga na kwingine kote maeneo mengi naamini, tumeona fedha kwa ajili ya kupeleka vifaa kwenye zahanati 300 na vituo vya afya 159, tunatamani sana tuone orodha hi ili tumshauri Mheshimiwa Waziri na tuhakikishe kila eneo limeguswa ili tuweze kuwa na maana nzuri hasa ya utekelezaji wa maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ningependa sana nizungumzie habari ya machinga. Sisi tunaotoka kwenye miji mikubwa, sisi tunaotoka kwenye majiji na nimwombe sana Mheshimiwa Waziri ameona juzi hapa kuna kitendo ambacho nashukuru Mungu sana alikiingilia haraka na sisi tukahakikisha kwamba haya siyo malengo ya Serikali, malengo ya Serikali ni kuwapanga wafanyabiashara kwenye maeneo mazuri, wafanye biashara ili waweze kujikwamua kutoka daraja moja kwenda daraja lingine. Kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Mkuu wangu wa Mkoa wa Mwanza kwa kuchukua haraka tukio la unyanyasaji la juzi ambalo lilikuwa siyo tukio zuri na naamini haya siyo malengo ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu sasa tunafikiria kwamba katika maeneo haya yote tunayoenda nayo, maeneo mengi tu wafanyabiashara wamekubali kwenda kwenye maeneo yao. Kwa mfano, nimepata milioni 500 kwenye Jimbo langu hii peke yake haitoshi kuwafanyia kuwatengenezea wafanyabiashara mazingira bora ya kukaa na kufanya biashara.

Mheshimiwa Spika, naomba waweke kipaumbele kwenye miji mikubwa Jiji la Mwanza, Mbeya, Dodoma, Tanga, Arusha, kama tumeamua kuwapanga watu hawa itengwe fedha maalum ya kuhakikisha tunaboresha maeneo. Halmashauri zetu Mheshimiwa Waziri hazijitoshelezi kuweka fedha ya kukarabati miundombinu yote. Tusukume fedha kwa wingi tuwasaidie vijana ili tuwawekee mazingira. Wamekubali kutoka barabarani na wanafanya vizuri sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: ...hata hivyo tuwalinde kwa sababu ni vijana wa Taifa la leo na tunawategemea sana.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa muda na Mungu akubariki sana nafahamu changamoto za Jiji la Mwanza ndizo changamoto za Jiji la Mbeya, kwa hiyo tushirikiane kuhakikisha kwamba vijana wetu na ndugu zetu wanafanya kazi vizuri na kusaidiwa sana. Mungu akubariki sana na ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. STANSLAUS S. MABULA - MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninakushukuru na ninaseme ahsante kwa fursa hii, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuisikiliza taarifa ya mwaka ya Kamati na ninatambua michango ya Wabunge mmoja mmoja kwenye hoja za Kamati na kwa kuwataja wachache ni kama ifuatavyo; Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani, Mheshimiwa Francis K. Ndulane, Mheshimiwa Jeremiah M. Amsabi, Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mheshimiwa Jesca J. Msambatavangu; na Mheshimiwa Mwita M. Waitara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wameonesha namna ubadhilifu wa fedha za umma unavyofanyika katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, wameonyesha kuwepo kwa upotevu wa fedha za umma katika mifumo ya kielektroniki ya mapato, manunuzi, mikataba na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati zinapokuwa zimepokea taarifa ya Mkaguzi ya CAG maana yake ni kwamba taarifa hii imepitia hatua nyingi sana ikiwemo kuzipa fursa Halmashauri ya kujibu hoja ambazo zimejitokeza wakati wa ukaguzi. Hoja wanapewa zaidi ya siku 21 wakati mwingine ili waweze kuzitolea majibu, inaposhindikana kabisa majibu yake hakuna bado wanapata nafasi na CAG anapokwenda anakuwa na vikao mbalimbali, kikao cha kwanza, anachofanya wakati anaingia lakini kunakuwa na kikao cha pili ambacho sasa kina mpa nafasi ya kuendelea na kazi yake, hata anapomaliza ndani ya siku 30 alizopewa bado atafanya exit meeting ambayo ataeleza kwenye eneo husika nini alichokutana nacho na atawaachia nafasi ya kujibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachojitokeza Halmashauri nyingi hazitoi majibu kwa wakati na hazitoi vielelezo vya maswali magumu waliyoulizwa na Mkaguzi. Lakini bado wanapata nafasi ya kuja mbele ya Bunge lako kwa maana ya Kamati ili waweze kuelezea na Bunge lako linatumia nafasi hiyo kuhoji likimhoji pande zote mbili kwa maana ya CAG lakini linawahoji pia watu waliokaguliwa, bado taarifa na majibu ya hoja zlilizotolewa hayapatikani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana taarifa zinazoingia hapa ndani kwenye bunge lako tunaamini ni taarifa zilizotenda haki kwa pande zote mbili na ni imani yetu kwamba Wakurugenzi na Watendaji Maafisa Masuuli wakifanya wajibu wao sawasawa inawezekana kabisa hoja hizi zikapungua sana na hizi sintofahamu, hii ni kweli au siyo kweli ikawa imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla Waheshimiwa Wabunge wamehimiza Serikali kuchukua hatua madhubuti dhidi ya ubadhirifu huo. Aidha Waheshimiwa Wabunge wameshauri Serikali kuzingatia utaalam katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo. Michango hii imeimarisha zaidi mapendekezo ya Kamati katika taarifa yake ya mwaka 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninahitimisha kwa kauli kwamba ubadhirifu katika mapato na matumizi ya fedha za umma ni jambo lisilostahili kufumbiwa macho, hivyo nalishawishi Bunge lako tukufu liunge mkono mapendekezo ya Kamati kuwa Maazimio ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivi tutasaidia sana iko mifano mingi kwa mfano, unakutana na hoja ya ukaguzi ambayo Mkaguzi amekuta Halmashauri Mtumishi aliyepaswa kulipa kwa mfano analipa Shilingi Laki Nne badala ya kulipa Shilingi Laki Nne anasema akaingiza namba ya simu ambayo tarakimu zake uki-count kwenye hela inakuwa, kwa mfano anaingiza namba 068… and so on, ambayo ukichukua 068 unatoa sifuri unazungumzia Milioni Mia Sita. Sasa cha kujiuliza kama yalikuwa ni makosa fedha hii imeingia kwenye account ya benki, baada ya masaa machache yaliyofuata fedha ile ile ya namba imeenda kutolewa benki kama cash money na kwenda sehemu ambayo haijulikani. Hizi ni moja ya changamoto ambazo ukweli zinaonyesha kabisa yako maeneo ambayo bado yanatakiwa kufanyiwa kazi, huu inawezekana ni utaalam mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri ya kuchukua hatua na kuendelea kufuatilia lakini tuna imani inawezekana mfumo wa TAUSI ukafanyiwa marekebisho zaidi na kutumia fursa na changamoto zilizojitokeza ili kudhibiti changamoto hizi za upotevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Ofisi ya CAG kwa kuwa jicho makini la Bunge katika hali kama hii, tuna imani Serikali itazidi kuiwezesha kifedha ofisi ya CAG ili kuwa na muda wa utekelezaji wa wigo mpana wa majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara nyingine tena nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge na naomba kutoa hoja.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hii Wizara muhimu kabisa ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, nimezisikiliza vizuri sana taarifa zote mbili. Nawapongeza sana Kamati ambayo imefanya kazi kubwa na taarifa yake iko wazi kabisa inajionesha. Vile vile nampongeza sana Waziri kwa taarifa yake ambayo hakika ametuonesha mwanga sisi Wabunge wenzake tunaowawakilisha Watanzania wengi wenye kiu ya kupata maji ya uhakika. Siku zote wanasema mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Mheshimiwa Aweso nakupongeza sana ndugu yangu, wewe pamoja na timu yako nzima Naibu wako, Katibu Mkuu. Hata yale makofi wakati wa utambulisho yalikuwa yanaashiria kazi nzuri mnayoifanya hasa kwenye upande wa usikivu na kutekeleza majukumu yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Rais; kwenye sekta ya maji ama hakika amefanya kazi kubwa ambayo inaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi natoka Kamati ya PIC. Tumekwenda kwenye Mikoa takribani mitatu kuangalia miradi ya maji ukiwemo Mkoa wa Arusha, Dar es Salaam, pamoja na Mwanza. Kazi ambayo inafanyika ni ya mabilioni ya fedha, lakini nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Wakurugenzi wa Mwanza (MWAWASA), Arusha (ARUWASA) pamoja na Dar es Salaam wa DAWASCO, wamefanya kazi nzuri sana ya usimamizi wa miradi mikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukizungumza Arusha, unazungumzia zaidi ya Shilingi bilioni 520; Mwanza zaidi ya Shilingi bilioni 69 mradi uko kazini, na Dar es Salaam vile vile.

Sasa nataka nizungumze mambo machache sana leo, lakini kubwa zaidi tuone namna gani tunavyoweza kuisaidia Wizara ya Maji katika kuhakikisha inatekeleza majukumu yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa wanayoitaka wananchi wetu kule tunakotoka ni kuona maji yanapatikana; maji, maji, maji. Yako maeneo kama Mwanza, tuna mahitaji ya maji zaidi ya lita milioni 160 kwa siku. Uwezo wetu kwa sasa ni lita milioni 90 peke yake. Hata hivyo, namshukuru sana Waziri na Mheshimiwa Rais kwa sababu hivi ninavyozungumza tunao mradi wa zaidi ya Shilingi bilioni 69 ambao unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwaomba sana wananchi wenzangu wa Jimbo la Nyamagana waendelee kuwa watulivu kwa sababu mradi huu utakapokamilika, utatusaidia kuongeza zaidi ya lita milioni 48 na kufanya tuzalishe lita milioni 138 kwa siku na tutabaki na upungufu wa lita milioni 22 peke yake. Hii ina maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba Wizara ya Maji kazi yake ni kuhakikisha fedha hizi zinapelekwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara ya Fedha kufanya kazi karibu sana na Wizara ya Maji, kwa sababu bila hivyo, leo inawezekana mkandarasi anataka fedha, lakini fedha kutoka Wizara ya Fedha; kuchukua fedha BoT na kuzifikisha kunakohusika, zinahitaji miezi miwili mpaka mitatu. Tunawakwamisha Watendaji wa Wizara ya Maji lakini tunakwamisha wananchi wetu kupata maji kwa wakati. Kwa hiyo, nawaomba Wizara ya Fedha tufanye kazi hii kwa muunganiko mkubwa ili kuweza kusaidia wananchi wetu walio wengi.

Mhshimiwa Spika, tumeona hapa bajeti imesomwa, Shilingi bilioni 657 fedha zinazokwenda kwenye miradi ya maendeleo. Nadhani Waheshimiwa Wabunge tunayo haja ya kutazama upya bajeti ya maendeleo ya maji. Fedha hizi ni kidogo sana ukilinganisha na mahitaji tuliyonayo kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupe mfano, baada ya Mheshimiwa Rais kupata fedha za UVIKO na kuamua kuzielekeza kwenye miradi ya maji, fedha nyingine, mimi peke yake Nyamagana nimepata karibia Shilingi bilioni moja, Mamlaka ya Maji ya Mwanza. Hii Shilingi bilioni moja imegawanywa Kata ya Ilemela na Nyamagana, lakini wananchi ambao ninawawakilisha leo maeneo ya Buhongwa kule Mitaa ya Ihila wamepata maji kwa sababu ya fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kule Butimba, Kambarage wamepata maji kwa sababu ya fedha hizi; ukienda Nyamazobe, Nyegezi wamepata maji kwa sababu ya fedha hizi. Maana yangu ni nini? Kama fedha hizi za UVIKO zimekuja kutuongezea tija kwa kiwango hicho, ni vipi tukiwa na uhakika wa bajeti yetu kutoka angalau Shilingi milioni 657 tukaenda Shilingi milioni 800 mpaka Shilingi milioni 900 na ikiwezekana hata tupate Shilingi trilioni moja kwenye miradi ya maji. Kama hatutawasaidia Wizara ya Maji kuwa na uhakika wa fedha za kutosha, tutaendelea kuomba fedha nyingine kutoka maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, ukiona hata miradi ninayoitaja leo ni fedha ambazo tunazipata kutoka kwa wadau. Tunayo miradi mikubwa ya Ziwa Victoria, tunategemea mradi wa Farkwa hapa, tumesikia hii EFDB wamepeleka fedha, lakini tunayo miradi mingine huko Dar- es-Salaam sijui Kidunda, Rufiji na kwingineko, hatuwezi kutekelea miradi hii kwa Shilingi Bilioni 657 peke yake. Maana yake ni nini? Turudi nyuma sasa, Mheshimiwa Rais ametembelea nchi nyingi, tumeona sasa hivi amekutana na wadau mbalimbali, anahamasisha watu kuja kuwekeza Tanzania na watu wamejitokeza, lakini kwa sababu watu wamejitokeza tutumie utaratibu ule ambao watu wengi wanakuja nao sasa hivi, watu wako tayari kuisaidia nchi na Wizara kupata fedha kwa ajili ya miradi ya maji. Tutumie utaratibu huo wa EPC ili kuhakikisha fedha hizi zinapokuja Wizara ya Maji inapokubaliana, Wizara ya Fedha iweke utaratibu mzuri watu hawa wapokelewe wakubaliane, waweke makubaliano sahihi na yenye tija kwa wananchi, fedha zipelekwe ili miradi hii tunayoizungumza mikubwa, huwezi kuhamisha maji kutoka Ziwa Victoria kuja Dodoma kwa kutegemea bajeti ya Wizara peke yake ya Bilioni 657, ni lazima sasa tufungue milango kwa sababu, Mheshimiwa Rais ameshatuonesha njia, ameshatufungulia njia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami nampongeza sana Mama huyu msikivu, Mama kipenzi huyu, Mama anayewapenda watu na amedhamiria kutusaidia hivi.

Mimi zamani nilikuwa simuelewi sana Mheshimiwa Aweso akisema wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani, nilikuwa najiuliza huu wali ukishauona unashibaje? Kumbe ukishauona wali kwenye sahani ndivyo appetite ya kula inavyozidi, ni sawa na wananchi wetu wanavyoona miradi mikubwa ya maji sasa hivi wanakuwa na matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Nyamagana kuna maeneo hawajawahi kufungua maji ya bomba, lakini leo kwa sababu kuna mradi wa Shilingi Bilioni 69 Butimba utakapokamilika mwakani mwezi wa Nne wananchi wangu wa kule Fumagila, mradi wa kule Rwanima, wa kule Nyamazobe, watakuwa na uhakika wa kuona maji ya bomba kwa mara ya kwanza. Kwa hiyo ni lazima tuwasaidie sana watu wa Wizara ya Maji. Mheshimiwa Aweso ni kijana kwa kweli anajitahidi sana, kwa umri wake na kazi anayoifanya anastahili pongezi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami nataka nikuhakikishie…

MHE. ERICK J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ERICK J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nataka kumpa tu taarifa mzungumzaji ya kwamba haya mambo yanayofanyika kwenye Jimbo la Nyamagana kule Buchosa kuna Bilioni 15 za mradi wa maji ambao unaendelea hivi sasa. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Stanslaus Mabula, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, naipokea Taarifa hii kwa mikono miwili. Na ninawaomba tu Waheshimiwa Wabunge…

SPIKA: Mheshimiwa una sekunde 30 malizia mchango wako.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, tumpe nguvu Mheshimiwa Aweso akafanye kazi hii kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kwa kunipa nafasi ya dakika hizi chache niweze kutoa mchango wangu kwenye wizara hii muhimu sana ya ulinzi wa Maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, na mimi nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Afya, Naibu Wake pamoja na Katibu Mkuu na Sekretarie nzima ya afya kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kusimamia Ilani ya Uchaguzi ambayo imeelekeza kuhakikisha ya kwamba Watanzania wanapatiwa afya na tiba ambazo zinalinda afya zao.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizi ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu maelekezo yake mengi yamekuwa yakifanyiwa kazi kwa usahihi. Pale Mwanza kwenye Jimbo la Nyamagana ambapo kuna Hospitali ya Mkoa wa Mwanza inayoitwa Seketoure, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu sasa baada ya kupata takribani shilingi bilioni 10 jengo limekamilika zaidi ya asilimia 98. Na hivi ninavyozungumza Mheshimiwa Waziri, leo narudia tena, niwapongeze sana kwa maamuzi mazuri yaliyofanywa na Mheshimiwa Rais zile fedha za UVIKO zilipelekwa kwenye maeneo ya afya ili kwenda kutatua changamoto vya vifaa.

Mheshimiwa Spika, Seketoure peke yake ilipata takribani bilioni mbili na milioni mia saba, Mheshimiwa Waziri kwa maelekezo imetumia zaidi ya asilimi 68, bilioni moja na milioni mia nane kununua vifaa vya lile jengo lote ulilolishuhudia pale, lakini asilimia 32 peke yake ndiyo imekwenda kwenye matumizi mengine ikiwemo nyumba ya muuguzi atakayekuwa anakaa pale, furniture na vifaa vingine.

Mheshimiwa Spika, sasa haya ni moja kati ya matokeo ambayo tunaamini wizara hii; Mheshimiwa Sekiboko amesema pale juu ya kulinda vifo vya mama na Watoto, na Mheshimiwa Waziri nikuhakikishie baada ya kuimarisha Hospitali ya Seketoure imeendelea kupunguza vifo vya mama na mtoto kutoka 18 mpaka vifo nane leo. Hatuna shaka ya kwamba vifo hivi vitaendelea kushuka sana kwa sababu ya uimarishaji bora wa huduma hizi za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwa haraka sana kwa sababu ya muda, ni kuhusu ulinzi na uimarishaji wa viwanda vyetu vya ndani vya dawa. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu alipotembelea pale MSD. Miongoni mwa mambo aliyoyapongeza ni kuona Kiwanda cha Keko Pharmaceutical pamoja na jitihada ndogo zilizokuwepo kimepiga hatua ya kuendelea kuzalisha dawa zinazohitajika ndani.

Mheshimiwa Spika, lakini nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, kiwanda hiki uwezo wake ni asilimia 36 peke yake. Tumekwenda pale na kamati yako ya PIC tumejionea shughuli na changamoto nyingi zilizokuwepo pale. Niombe, MSD, Keko Pharmaceutical wanahitaji bilioni 12 peke yake ili wafikie uwezo wa dawa zote 10 zinatakiwa hapa.

Mheshimiwa Spika, na nimpongeze sana mkurugenzi mpya wa MSD, ninaamini Serikali, Waziri Mheshimiwa Ummy na Serikali mmefanya nafasi yenu. Hili wala si la kufumbia macho, popote jicho lako linapokwambia kuna shida inaweza kukwamisha maendeleo ya sekta ya afya chukua maamuzi na amua mara moja ili tuweze kutoa tija kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunamkurugenzi mpya MSD, sina shaka na yeye atakuwa na nafasi yake kwenye maeneo ya ndani ya utawala wake. Na Mheshimiwa Waziri tukifumbiana macho katika sekta ya afya ambayo ni moja ya sehemu ya ulinzi wa taifa hili hii ni zaidi ya kiwanda cha mabomu. Mheshimiwa Waziri usipolinda sekta ya afya vizuri nataka nikuhakikishie watu wako watakufa kwa magonjwa, watu wako watashindwa kupata tiba na sisi tutakuwa hatuna maana ya kuwepo hapa ndani kwa sababu moja ya jukumu letu ni kuwapa nguvu viongozi mliopewa nafasi ya kusimamia sekta hii; na sisi tunawaunga mkono tunaamini sasa changamoto zote zilizokuwepo MSD zitakwisha na hata hiki kiwanda cha Keko.

Mheshimiwa Spika, tumetembelea pale sisi, meneja anayekisimamia na wasaidizi wake wengi wote ni akina mama. Kwa hiyo, tunaamini akina mama katika ile eneo la kusimamia kazi zenu kwa nguvu mkurugenzi atasimamia na atafanya kazi yake vizuri. Tunataka tuione MSD kwenye kiwango cha kimataifa. Tupate ithibati ili tuuze dawa mpaka kule kwenye nchi za SADC kwa kufanya hivyo itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine tunaomba kufahamu, Mikoa ya Kanda ya Ziwa sasa hivi ugonjwa wa kansa umeendelea kuwa mkubwa sana. Mimi niwapongeze, sana mlipoweka nguvu kuhakikisha Hospitali ya Bugando inajenga jengo kwa ajili ya wagonjwa maalumu wa kansa, na sasa hivi jengo hili lipo takribani asilimia 98. Watu wa Bugando wamesimamia vizuri; na nimpongeze sana Mkurugenzi wa Bugando na timu yake nzima. Unajua watumishi wa afya hawa pamoja na changamoto nyingi tulizonazo lakini hakika wanajitahidi kufanya kazi yao vizuri na wanastahili sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jengo hili la Bugando kukamilika kwake tunahitaji vifaa; kwenye bajeti yako hakikisha kadiri unavyoweza. Niwapongeze kwa sababu mmeshaanza na Ocean Road. Mmeweka kiwanda ambacho viwanda vya aina hii katika Afrika vipo vinne peke yake; na sisi dawa zote tunategemea Afrika Kusini. Leo tukiongeza cha kwetu kitakuwa cha tano katika Afrika. Maana yake ni kwamba, sasa ukiongelea lile suala la Mama anaupiga mwingi ulitazame kwenye angle hii, ambayo inakwenda kuokoa maisha ya wananchi wengi wa kanda ya ziwa; na kwa kufanya hivyo mtakuwa mmelisaidia sana taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya mambo tunayoyasema si mambo mepesi. Wenzangu wameongea hapa juu ya mfumo wa ulinzi wa mapoteo ya pesa za NHIF. Leo ukitibiwa Bugando au Seketoure ukapata referral kwenda Muhimbili ukifika kule unaenda kuanza upya. Kumbe kungekuwa na mifumo hii ambayo inasomana vizuri ingekuwa ni rahisi daktari aliyepo kule Muhimbili kuona taarifa zako za Bugando na akawa na ulinzi mzuri kwa ile kadi na fedha ambayo mnaitoa ya NHIF. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, najua kengele imegonga, hasa kwa sababu nilikuwa kwenye moto sijui ni ya pili sijui ni ya kwanza.

SPIKA: Ya pili Mheshimiwa.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, lakini niwaombe Waheshimiwa Wabunge tumpe ushirikiano wa kutosha Mheshimiwa Waziri tuipe ushirikiano wa kutosha Wizara hii, Katibu na timu yake nzima. MSD pia tuipe nguvu ili ifanye kazi vizuri.

SPIKA: Haya, ahsante sana.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. STANSALUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba nitumie fursa hii kwanza kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi. Vilevile nimshukuru sana Mungu wetu wa Mbinguni anayeishi kwa kuendela kutupa uhai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitazungumza maneno machache sana. Nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, na katika ile hesabu ambayo Mheshimiwa Waziri ameitaja ya maika miwili ya mafanikio kwenye sekta ya maji ya Mheshimiwa Rais, sisi watu wa Nyamagana Pamoja na Jimbo la Ilemela kwa mama yangu pale Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula tunayo kila sababu ya kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa sababu katika mafanikio ya miaka miwili Nyamagana tunaenda kuopata chanzo kingine kipya cha maji baada ya miaka 43.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tupigie mstari baada ya miaka 43 iliyopita ndipo tunaenda kupata chanzo kingine cha maji. Lakini pale Ilemela tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu pale Kabangaja tunategemea kuwa na chanzo kingine cha maji, tangu Ilemela imeanza, tangu Mwanza imekuwepo. Tafsiri ya vyanzo hivi viwili ni kwenda kupunguza au kuondoa kabisa tatizo la maji kwenye Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela. Kwa hiyo tunamshukuru sana Rais na namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu, yeye ndiye anayelala na mgonjwa na kwa sababu yeye ndiye anayelala na mgonjwa anajua matatizo mengi. Nimpongeze yeye na timu yake kwa sababu, ya kuokoa muda. Kila aliyeko kwenye Wizara ya Maji atambue kwamba, nimempongeza kutokana na kazi kubwa wanayofanya, wakiongozwa na Waziri mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Nasema hivi kwa sababu nchi hii, wamesema pale Mheshimiwa Hokororo na Mheshimiwa Engineer Ulenge, tumekuwa na matatizo ya maji toka miaka mingi iliyopita. Nikizungumza leo Nyamagana hapa, miaka 43 iliyopita tulikuwa tunategemea chanzo kimoja peke yake kilichojengwa miaka ya 80 kikiwa na uwezo wa kuhudumia watu laki moja peke yake. Leo, miaka 43 baadaye tunazungumza chanzo kipya kinachojengwa kitakuwa na uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 48 kwa siku na kitahudumia ongezeko la watu zaidi ya 105,000. Hapa nataka kusema nini Mheshimiwa Aweso? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika pamoja na changamoto nyingi tulizonazo, safari aliyoianza Waziri toka amekuwa kwenye Wizara hii, sisi wenzake inatupa matumaini na faraja ya kwamba, iko kazi kubwa anayoifanya na Wizara yake. Nina hakika ni lazima tumuunge mkono na kumtia moyo kwamba, miradi ya maji siyo sawa na ujenzi wa nyumba, unaweza kufikiri asubuhi, ukajenga jioni, kesho umekamilisha na matokeo yakaonekana. Kazi kubwa anayoifanya ndio itakayotupa sisi dira ya kule tunakokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Nyamagana kama nilivyosema, chanzo chetu cha kwanza kimejengwa miaka ya 80. Leo tunaongeza lita milioni 48 kwenye chanzo kipya, naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita, mpaka hivi tunavyozungumza Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake umesema mwenyewe tuko takribani asilimia 71. Ukweli usiopingika, kukamilika kwa chanzo hiki itakapofika Julai, tarehe 30, tutakuwa tumefanikisha kupata lita zipatazo jumla yake Kapri Point na Butimba zitakazofikia milioni 148 peke yake. Bado tunahitaji lita milioni 22 ili kuwahudumia wananchi wa Jimbo la Nyamagana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoutaja mradi huu Mheshimiwa Waziri akumbuke ndio utakaowasaidia watu wa Magu na Misungwi, lakini maeneo yetu yote kwa sasa ambayo yanapata changamoto ya maji, ukienda kule Buhongwa, Rwanima, Kishiri, Igoma, Nyegezi, Mkolani, Luchelele, kote huko changamoto hii inategemea kukamilika kwa chanzo hiki. Sasa ushauri wangu Mheshimiwa Waziri; tunafahamu, Ilemela nimetaja chanzo cha Kabangaja, Nyamagana tunacho chanzo cha Capri Point, ili tuweze kuwa na uhakika wa maji kwa wakazi wetu wote kwa maeneo haya, tunahitaji uzalishaji wa chanzo cha Kabangaja pale kwenye Manispaa ya Ilemela, lakini tunahitaji uboreshwaji wa chanzo cha Butimba kitoke kuzalisha lita milioni 48 kwa siku mpaka lita milioni 160 ili tuweze kufikia malengo ambayo tumekubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu na kila mmoja anajua Serikali yetu bado ni himilivu sana kwenye ukopaji na bado inazo sifa za kuendelea kukopa. Kama tuna uwezo wa kukopa au kushawishi na kushirikisha mashirika mbalimbali, kama tulivyofanya kwenye huu mradi ulioko Nyamagana leo, tuendelee kuchukua fedha kwa sababu, tukikamilisha miradi hii tutakuwa tumeliokoa Taifa hili, tumewasaidia wanawake wa Taifa hili, tumeimarisha ndoa kama wanavyosema akinamama za Taifa hili na tumejenga umoja kwenye Taifa hili kwa sababu, tutakuwa na uhakika wa maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine kadri tunavyofanya nusunusu tafsiri yake ni kwamba, leo tumelaza bomba kilometa 17 kutoka Butimba kwenda Sahwa ambapo maji yatakuwa yanapokelewa kutoka kule Butimba, lakini kutoka Sahwa kwenda Igoma kwenye tenki linalozalisha lita milioni tano. Maana yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukilazimika kuja kuongeza miaka miwili baadaye itatulazimu kuweka mfumo mpya wa ulazaji bomba, ili liweze kuendana na chanzo tutakachokuwa tumekijenga. Tukikamilisha vyanzo hivi sio mbaya, tunahitaji takribani bilioni 400 kwa mujibu wa wataalamu walivyofanya na bilioni 400 sio nyingi kwenye kuzalisha maji kwa sababu, Mamlaka ya Maji ya MWAWASA inao uwezo mkubwa wa kujiendesha yenyewe kama itakuwa na uhakika wa kusambaza maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, watendaji wake wote wa Mamlaka ya Maji ya MWAWASA, nafahamu wananchi wa Nyamagana wanazo changamoto, lakini hakuna safari tunayoweza kufika bila kutembea. Hakuna safari tunayoweza kufika bila kuchukuliana. Kazi hii ni kubwa, haijaanza leo na ndio maana nimesema, Waziri Mheshimiwa Aweso chini ya Serikali ya Awamu ya Sita anaingia kwenye rekodi ya Jimbo la Nyamagana na Wilaya na Jiji la Mwanza kwa kuwa wa kwanza kuhakikisha chanzo cha lita milioni 48 kinajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina shaka kazi hii aliyoianza kwa muda mrefu itawasaidia sana, lakini hatuwezi kukamilisha chanzo peke yake bila kukamilisha maeneo yatakayopokelewa maji na usambazaji. Nafahamu tunatarajia au tunakusudia kujenga tanki moja kule Rwanima, Mtaa wa Kagera, litakalobeba lita milioni 10, lakini kule Rwanima yenyewe lita milioni tano, Mtaa wa Kasese kule Mkolani lita milioni tano, ili tuweze kuwahudumia watu wa Luchelele. Pale tuna Chuo cha SAUT peke yake kinahitaji maji yasiyopungua lita milioni 10 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri alitazame Jiji la Mwanza ambalo ni kilometa zisizopungua saba kutoka kwenye maji mpaka kwenye chanzo na usambazaji wake, ukichukua eneo lote la Nyamagana, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri ni eneo ambalo linawezza likatushangaza na likatuletea mapato mengi kupitia Mamlaka ya Waziri ya Maji na akafanya kazi nyingine na mamlaka hii inaweza kusaidia kuzalisha fedha zitakazotoa huduma kwenye maeneo mengine. Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumeupiga mwingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kusema nampongeza sana Mheshimiwa Aweso. Miradi ya maji ni safari na safari hii ameianza vizuri na anaenda nayo vizuri, ni wajibu wetu kumuunga mkono, ni wajibu wetu kumuunga mkono sana Mheshimiwa Rais kwa sababu, malengo na mafanikio yanaonekana. Mabadiliko tunayoyaona kwenye bajeti ya kila mwaka ndio tafsiri ya utekelezaji na matokeo yake. Nimshukuru sana na nimpongeze, watu wa Nyamagana wanamsubiri Waziri kwenye uzinduzi wa chanzo hiki cha maji pamoja na Mheshimiwa Rais, ili waje waone faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe babu, unajua Waziri Mheshimiwa Aweso ni babu yetu, unajua Waziri ni mjukuu wa Wasukuma, kwa hiyo, kila analolifanya ahakikishe babu zake wasimtie laana mzee na safari hii umepata Naibu Katibu Mkuu hapo na yeye ni mjukuu wake, kwa hiyo, ahakikishe kazi hii inakwenda vizuri sana. Mungu awabariki sana, nawashukuru sana, ahsanteni. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi angalau kwa dakika chache niweze kusema mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mungu kwa kunipa nafasi lakini la pili na mimi nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ya kipekee ambavyo amekuwa mtu mwema sana katika kuhakikisha kwamba fedha nyingi zinazokwenda kwenye miradi zinasimamiwa na zinatekeleza miradi ambayo imekusudiwa. Na hakika, kama mwenyewe anavyosema, hakuna mradi uliosimama kila mradi uliokusudiwa unaendelea na tumekuwa na miradi bora sana. Nimshukuru kwa kuhakikisha ya kwamba tunavyozungumza kama wenzangu waliokwisha kupita wamesema; ukitazama Daraja la Busisi ambalo linaunganisha Mkoa wa Mwanza na mikoa mingine ya Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pale kwenye bandari utakuta kuna meli kubwa ambayo itakuwa ni meli ya kipekee katika ukanda wa maziwa makuu; MV. Mwanza, ambayo kwa hakika iko hatua za mwisho kabisa kukamilika. Ukitazama standard gauge ambayo inaanzia Mwanza kwenda isaka nataka nikuhakikishie kwamba miradi hii yote inatekelezeka na iko, wakandarasi wako kazini, na hakika wanafanya kazi nzuri sana. Ba hii peke yake imefanya Mji wa Mwanza kuwa busy, Mji wa Mwanza kuwa mji ambao unampishano wa watu kila mara na kwa wingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? tafsiri yake ni kwamba uchumi unaojitokeza kwenye uendelezaji wa miradi unaotoa ajira nyingi kwa vijana tafsiri yake ni kwamba kukamilika kwa miradi hii kunaifungua mkoa wa Mwanza kunaifungua Kanda ya Ziwa na kufanya sasa mji huu uendelee kuwa mji wa pili mashuhuri na kwa ukubwa katika nchi hii katika kuhakikisha kwamba miradi hii inakuja kuleta tija kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusudi hilo nataka nimuombe Mheshimiwa Waziri mambo mawili peke yake. Kama tunazungumzia miradi yote hii na haina muda mrefu inakwenda kukamilika tunao Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, unapozungumza ujenzi wa Daraja la Busisi, unapozungumza ujenzi wa SGR kutoka Mwanza kwenda Isaka unapozungumza uboreshaji wa bandari na ujenzi wa meli kubwa tafsiri yake ni kwamba Mji wa Mwanza unakwenda kuwa mji wa kitalii lakini unakwenda kuwa mji wa biashara asilimia 100. Hivyo nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, ninafahamu, ujenzi wa uwanja wa ndege, njia ya kukimbila ndege imeshakamilika lakini hivi tunavyozungumza ni aibu sana kuendelea kusema tuna jiji la pili kwa ukubwa lakini bado tuna uwanja wa ndege unaoweza kupokea ndege za kwetu za ndani peke yake na si ndege za mashirika mengine makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafahamu Halmashauri za Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela zilianza mchakato wa ujenzi wa jengo la abiria lakini ukweli, ni kwamba Mheshimiwa Waziri na wewe utakubaliana na mimi haiwezekani imefika sehemu zimegota na sio jukumu lake kimsingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukuombe Mheshimiwa Waziri kama ambavyo tumekwisha kuzungumza uwanja huu wa ndege urudi TAA usimamiwe na wataalamu wenyewe na hazi halmashauri mbili kwa sababu mpaka sasa zimeshagharamia takribani shilingi bilioni nne fedha hii baada ya kuwa uwanja huu umerudi na jengo hili limechukuliwa zitatazamwa kwenye namna nyingine ili ziweze kupata share na zenyewe ziweze kufaidika na mapato haya ya ndani kwa sababu ni kodi za wananchi zimepelekwa pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunasema uwanja wa ndege wa Mwanza? Leo ukitazama unapokea abiria zaidi ya milioni moja kwa mwaka lakini majengo yanayosubiri abiria, maeneo ya kupumzika, maeneo ya kusubiri kuondoka na kuingia hakika hayafanani kabisa na ule uwanja ulivyo hivyo nikuombe sana Mheshimiwa Waziri halmashauri hizi zimesharidhia ziko tayari ni kazi kwako kuhakikisha ya kwamba uwanja huu unauchukua na unauboresha kwenye mazingira ambayo yatafanya uwe uwanja wa kimataifa ndege kubwa zije ili na sisi tuweze kuona faida ya kuruka kutoka Mwanza moja kwa moja kwenda Dubai na maeneo mengine duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu barabara, Mheshimiwa Waziri unafahamu tunayo barabara moja kubwa ya Kenyatta na ya Nyerere. Barabara ya Nyerere na ya Kenyatta ni barabara ambazo zinapitisha abiria wengi sana ukiitaja kwa mfano barabara ya kenyatta peke yake abiria wote wanaoingia Mwanza kutokea Mikoa ya Dar es salaam na mikoa mingine yote ikiwemo mikoa inayounganishwa na Daraja la Busisi wanatumia barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni nini? Barabara hii imekuwa finyu na haina tena uwezo wa kuwahudumia wakazi wanaokuja Mwanza. Kwa hiyo ninachokuomba Mheshimiwa Mbarawa barabara hii ilishafanyiwa upembuzi yakinifu kwa njia nne na ulishakamilika siku nyingi, basi tuitazame kwa jicho la pekee na tuanze kuijenga angalau hata kwa kilometa kumi kwa mwaka wa fedha ujao, itakuwa imesaidia sana kuondoa changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakazi peke yake wa Mwanza wanaokadiriwa laki sita na sehemu nusu ya wakazi wa Mwanza wanatumia barabara hii, hapo hujawataja wageni. Barabara ina uwezo wa kuchukua magari zaidi ya 3,000 mpaka 6,000 kwa siku hii siyo jambo dogo, ni jambo kubwa, hivyo ni lazima tulitazame kimahesabu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hiyo tu, Mheshimiwa Waziri tumezungumzia namna ya kuipandisha hadhi barabara inayotoka Mkuyuni inapita Kanyenyere inakwenda Tambuka Reli inakwenda mpaka Nyanguruguru inakwenda kutokea Mandu na Mahina. Barabara hii ni muhimu sana kwa wakazi wa Jiji la Mwanza na ni muhimu sana kwa Mkoa wa Mwanza kwa sababu itasaidia kwenye maeneo mengi ambayo tunayategemea mno kwa ajili ya kuwavusha wananchi kwenda kwenye shughuli zao za kiuchumi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja, na ninaipongeza Wizara ya Ujenzi na taasisi zake zote kwa kazi nzuri wanayoifanya, na Mungu aendelee kuwasaidia kulitumikia Taifa. Ahsante sana. (Makofi)