Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Ester Michael Mmasi (13 total)

MHE. ESTHER M. MMASI aliuliza:-
Serikali kupitia taasisi za umma zimeweza kufanya tafiti nzuri kujua uhalisia wa suala la ajira kwa vijana waliohitimu vyuo vikuu:-
Je, ni kwa namna gani Serikali inaweza kutumia majibu ya tafiti hizo kupitia convocation office ndani ya taasisi ya umma katika kutatua changamoto za ajira katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU (MHE. ANTONY P. MAVUNDE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara imekuwa ikifanya au kutumia tafiti zilizokwisha kufanywa na taasisi mbalimbali ili kushughulikia changamoto za ajira, upangaji wa mipango na utatuzi wa changamoto za ajira kwa vijana wa vyuo vikuu na wengineo.
Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa na tafiti hizo zinasaidia Serikali kupanga na kutekeleza mikakati ifuatayo:-
(i) Programu ya Kukuza Ujuzi inayolenga kuwapatia wafanyakazi na vijana maarifa na stadi za kazi ili waweze kuajirika na kujiajiri.
(ii) Mfuko wa wa Maendeleo ya Vijana unaolenga kuwapatia vijana mafunzo na mikopo nafuu ya kujiajiri. Mfuko unawahamasisha wahitimu kuanzisha vikundi vya uzalishaji na makampuni ili wajiajiri na kuajiri wengine.
(iii) Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambalo linadhamini wahitimu wachanga kupata mikopo nafuu katika Benki ya Uwekezaji Tanzania (TIB) kwa njia ya ushindani ili waweze kufanya shughuli za kujiajiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki ya uwezeshaji kwa vijana na wahitimu wa vyuo vikuu ili kutatua changamoto za ajira katika nchi yetu kwa kushirikiana na wadau husika kama waajiri, taasisi za elimu, taasisi za kifedha na vijana.
MHE. ESTER M. MMASI aliuliza:-
Changamoto nyingi kwa upande wa kada za waendeshaji Vyuo Vikuu unatokana na uteuzi usio na tija katika nafasi za Wakuu wa Vitengo, Rasilimali Watu na uongozi chini ya Mwongozo wa Universities Charter.
Je, nini msimamo wa Serikali kuhakikisha kada za watumishi wa umma, Taasisi za Elimu ya Juu zinaheshimika na nafasi za Wakuu wa Vitengo, Rasilimali Watu, zinatumika kiufasaha kulingana na miongozo ya kiutumishi.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uteuzi wa kada za waendeshaji pamoja na Wakuu wa Idara na Vitengo katika vyuo vikuu vya umma hufuata muundo wa utumishi wa wafanyakazi waendeshaji ambao pamoja na mambo mengine, unazingatia miongozo inayotolewa na Serikali kupitia Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mheshimiwa Spika, nina imani kwamba tatizo siyo taratibu, sheria au miongozo iliyopo ya uteuzi kama hati idhini za vyuo vikuu (universities charter), bali ni ukosefu wa maadili ma ubinafsi kwa baadhi ya wahusika kwenye michakato hiyo. Serikali imeshachukua hatua ya kuchunguza malalamiko kama hayo katika vyuo na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sanyansi, na Teknolojia ili kujua ukweli na ikibainika kuwa kuna wahusika walivuruga utaratibu na kupelekea kuteuliwa viongozi wasiostahili watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-
Pamoja na juhudi za Serikali katika kulinda ajira za vijana wa Kitanzania, Serikali kupitia Sheria ya Ajira ya Wageni Na. 1 ya mwaka 2015 ilirasimisha vibali vya kuishi na ajira kwa wageni batili wapatao 317 kati ya 779.
Je, ni vigezo gani vilivyotumika katika urasimishaji wa vibali hivyo wakati vijana wengi wa Kitanzania hususan wahitimu wa vyuo vikuu wanahangaika katika kupata ajira ili wafurahie faida ya taaluma zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Kuratibu Ajira kwa Wageni Nchini Na.1 ya mwaka 2015 ilianza kutumika tangu tarehe 15/9/2015. Sheria hii imeweka utaratibu maalum kwa mtu anayetaka kumuajiri raia wa kigeni kuomba kibali cha ajira kwa Kamishna wa Kazi ambaye ndiye mwenye mamlaka pekee ya utoaji wa vibali vya ajira kwa wageni nchini. Kamishna wa Kazi alianza kazi ya kutoa vibali kwa wageni kuanzia tarehe 1/10/2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, vigezo vinavyotumika kurasimisha vibali kwa wageni vimeainishwa katika kifungu cha 6(1) katika Sheria ya Kuratibu Ajira ya Wageni Na.1 ya mwaka 2015 ambapo masharti mbalimbali yameainishwa kwa mwombaji kukidhi kabla ya Kamishna wa Kazi hajatoa vibali. Mojawapo ya sharti ni kumtaka mwajiri atoe ushahidi wa kuridhisha kwamba ametafuta mtaalam huyo kwenye soko la ajira la ndani na hakupata mtu mwenye sifa husika na vilevile azingatie suala la mpango wa urithishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inapenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa itaendelea kusimamia Sheria hii Na.1 ya mwaka 2015 ili kulinda nafasi za ajira za Watanzania wenye fani na taaluma mbalimbali.
MHE. ESTER M. MMASI aliuliza:-
Kupitia fursa ya ujenzi wa bomba la mafuta Mkoani Tanga, ni dhahiri kwamba vijana takribani 15,000 watapata ajira kwenye mradi kwa upande wa Tanzania:-
(a) Je, Serikali imejipangaje kuona kuwa vijana wa Kitanzania wanapata ajira katika soko la Tanzania kupitia fursa hii ya uwekezaji?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuingiza mtaala wa mafuta na gesi katika mitaala ya VETA ili kuwajengea uwezo, maarifa na ujuzi vijana wa Kitanzania katika sekta hiyo muhimu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi Bandari ya Tanga (Tanzania) uko katika hatua ya majadiliano ya jinsi mradi huo utakavyotekelezwa. Katika majadiliano hayo, suala la ajira kwa Watanzania litazingatiwa ili Watanzania wanufaike na ajira kupitia ujenzi na uendelezaji wa mradi huo. Mradi unatarajiwa kutoa ajira 10,000 wakati wa ujenzi na ajira kwa watu 1,000 wakati wa uendeshaji.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 na 2013 Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na Kampuni ya Petrobras ya Brazili, iliendesha mafunzo maalum ya ufundi wa plumbing, uchomeaji, upakaji rangi pamoja na mambo mengine katika Chuo cha VETA huko Mtwara na Lindi. Mafunzo hayo yalilenga kuwaongezea weledi wanafunzi wapatao 350 wa VETA ambao wamepatiwa vyeti vya kimataifa na wanaweza kuajiriwa ndani ya nchi na nje ya nchi. Gharama za mafunzo yote ni Dola za Marekani milioni nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Serikali ya Norway, chini ya Mradi wa Mafuta kwa Maendeleo (Oil for Development) imekamilisha taratibu za kuingiza mtaala wa mafuta na gesi katika vyuo vya VETA hapa nchini. Mtaala huu utaanza kutumika katika baadhi ya vyuo vya VETA hapa nchini mwaka 2018. Utekelezaji wa mpango huu utagharimu Dola za Marekani milioni 20.
MHE.ESTHER A. MAHAWE (K.n.y. MHE. ESTHER M. MMASI) aliuliza:-
Kupitia fursa za ujenzi wa mabweni ya wanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwezi Aprili, 2017.
Je, Serikali imeweka jitihada gani katika kuongeza fursa za ujenzi wa mabweni kwa Taasisi za Elimu ya Juu hususani Chuo cha Ushirika Moshi Mkoani Kilimanjaro ambapo zaidi ya 70% ya wanafunzi wanaishi nje ya chuo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika vyuo vikuu nchini, Serikali imewezesha ujenzi wa mabweni mapya 20 katika chuo kikuu cha Dar es Salaam vyenye uwezo wa kubeba wanafunzi 3,840 na kukamilisha ujenzi wa Chuo Kikuu cha Taaluma cha Tiba (MUHAS). Aidha, Serikali imefanya juhudi za kuainisha hali ya miundominu katika vyuo vya elimu ya juu ili kubaini mahitaji halisi. Baada ya tathmini hiyo, kupitia Mradi wa Malipo kwa Matokeo (P for R) Serikali imeanza ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya vyuo vikuu vya Sokoine, Dares Salaam, Ushirika Moshi na Mzumbe.
Mheshimiwa Spika, Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi kina hostel zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 900 kwa wakati mmoja, idadi hii ni sawa na asilimia 25% ya wanafunzi wote. Ili kuhakikisha mazingira bora ya malazi kwa wanafunzi, chuo kina mpango wa kujenga hostel zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 3,500 kwa wakati mmoja. Mpango huu umebainishwa katika mpango mkakati wa chuo wa miaka mitano.
Mheshimiwa Spika, aidha, kwa mwaka wa fedha 2017/2018 chuo kupitia miradi ya maendeleo ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kinategemea kupatiwa fedha za ujenzi wa hostel zenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,000 kwa wakati mmoja. Ujenzi huu ukikamilika utasaidia kutatua kwa kiasi kikubwa tatizo la malazi kwa wanafunzi na hivyo kuchangia katika kufanikisha azma ya Serikali ya kuzalisha wataalam wengi. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-
Serikali imekuwa na juhudi mbalimbali za kuinua kiwango cha ajira zisizo rasmi nchini.
Je, nini mpango wa Serikali katika kuwawezesha vijana wahitimu waweze kuingia rasmi kwenye sekta ya kilimo na ufugaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu Swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali katika kuwawezesha vijana wahitimu waweze kuingia rasmi kwenye sekta ya kilimo na ufugaji ni kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kutekeleza mkakati wa Kitaifa wa kukuza ujuzi nchini ambao umelenga kutoa mafunzo ya kukuza ujuzi kwa wahitimu, wakiwemo wale wanaopenda kujiunga katika kilimo na ufugaji. Kupitia programu hii ofisi yangu imetenga fedha kuwezesha vijana, wakiwemo wahitimu, kupatiwa mafunzo ya kilimo cha kutumia kitalu nyumba (green house). Mafunzo haya yatafanyika katika Mikoa yote Tanzania Bara na tayari tumetoa maelekezo kwa Ofisi za Mikoa kuhamasisha vijana kujiunga katika vikundi kwa lengo la kuwawezesha kupatiwa mafunzo hayo katika maeneo maalum yaliyotengwa na mikoa yao kwa shughuli za vijana.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kuboresha mazingira bora ya uwekezaji katika sekta zenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira, hususan kilimo biashara. Aidha, katika hili Serikali itajikita zaidi kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji kwenye viwanda vidogo vidogo, vya kati na vikubwa, ili kufikia lengo la asilimia 40 ya nguvu kazi nchini kuwa katika sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2020. Kupitia Mpango wa Pili wa Maendeleo wa miaka mitano, mwaka 2016/2017 na mwaka 2020/2021.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendelea kuimarisha utekelezaji wa mfumo wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na mifuko mingine ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, ambayo inalenga kuwasaidia vijana kuweza kujiajiri na kuajiri wenzao kwa kuwapa mikopo yenye masharti nafuu na mafunzo ya ujasiriamali kupitia kwenye SACCOS za Vijana ambazo zimesajiliwa. Aidha, Serikali kupitia Halmashauri zote nchini inaendelea kuhamasisha kutengwa kwa asilimia tano ya mapato yake kwa ajili ya kuwakopesha vijana, ili kujiajiri na kuajiri vijana wengine.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-
Baadhi ya vyuo vikuu nchini vimekuwa na utamaduni wa kutozingatia miongozo ya Serikali Kuu katika kuongoza na kusimamia vyuo vikuu nchini na hata kupeleka kupuuzwa kwa stahiki za wafanyakazi wa elimu ya juu kwa kisingizio cha elimu ya juu inajiongoza na kujisimamia yenyewe chini ya University Charter:-
Je, ni nini kauli ya Serikali katika hili?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uendeshaji na usimamizi wa elimu ya juu nchini unasimamiwa na Sheria ya Vyuo Vikuu, Sura 346 na Kanuni zake za mwaka 2013. Kupitia sheria hiyo, vyuo vikuu vyote nchini vinaelekezwa kuweka mifumo ya usimamizi wa vyuo na kuunda Mabaraza na Kamati za Kitaaluma ili kuhakikisha kuwa usimamizi wa taaluma vyuoni unaenda sambamba na ubora unaotarajiwa. Hivyo, hakuna chuo chenye Hati Idhini (University Charter) ambayo inatekelezwa kinyume na sheria hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napenda ifahamike kwamba msimamizi mkuu wa Sheria ya Vyuo Vikuu ni Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) ambayo imepewa jukumu kisheria kusimamia ithibati na udhibiti ubora wa elimu ya juu nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TCU imekuwa na utaratibu wa kufanya ukaguzi wa vyuo vikuu mara kwa mara ili kuona kama vinazingatia sheria, taratibu, kanuni na miongozo ya uendeshaji kulingana na madhumuni ya uanzishwaji wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TCU imetoa Miongozo ya Ajira kwa Wafanyakazi wa Vyuo Vikuu nchini yaani Minimum Guidelines For Employment, Staff Performance Review and Career Development, 2014 ambayo inatoa dira kuhusu ajira (recruitment), upandaji vyeo (promotion) na uwiano wa kazi (workload) ambazo waajiri wa vyuo vikuu wanatakiwa kuzingatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine chuo kikuu kinapobainika kukiuka sheria, taratibu, kanuni na miongozo iliyopo, hatua za kinidhamu zimekuwa zikichukuliwa mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na sheria hii, ajira katika vyuo vikuu husimamiwa pia na sheria nyingine zinazohusu kazi na ajira hapa nchini. Hivyo, kama kuna malalamiko yoyote kuhusu watumishi kutopatiwa haki zao za ajira katika baadhi ya vyuo vikuu yawasilishwe Serikalini kwa ajili ya kufanyiwa kazi.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-
Kituo cha Afya Wilaya ya Siha kimeonekana kukidhi mahitaji yote muhimu tayari kwa usajili lakini hadi sasa kituo hicho hakijapata usajili wa Hospitali ya Wilaya.
Je, ni nini kauli ya Serikali katika kupandisha hadhi kituo hicho ili kupunguza kadhia ya upatikanaji wa huduma za kiafya kwa wananchi wa Wilaya ya Siha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuanzishwa Wilaya ya Siha haikuwa hospitali ya wilaya, hivyo Kituo cha Afya Siha ndicho kilichotumika kutoa huduma za matibabu kwa ngazi ya Hospitali ya Wilaya. Mwaka 2009/2010 Wilaya ya Siha ilipata eneo ambalo lilitolewa na vyama vya ushirika viwili ambavyo vilitoa jumla ya ekari 40 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, hii ilitokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Siha na hivyo kushindwa kumudu idadi ya wagonjwa na kupelekea uhitaji wa uanzishwaji wa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na wadau wengine wa maendeleo walisaidia uanzishwaji wa ujenzi wa Hospitali ya Wilayana kufikia kuanza kutoa huduma za afya. Hospitali inapokea wagonjwa wa rufaa kutoka katika vituo 20 vya kutolea huduma za afya vikiwemo vituo binafsi, vituo vya mashirika ya dini pamoja na vituo vya Serikali. Lengo la Serikali si kukipandisha hadhi Kituo cha Afya Siha kuwa Hospitali ya Wilaya, bali kuendelea kuboresha miundombinu inayoendelea kujengwa katika Hospitali ya Wilaya ili kuwa na hadhi kamili ya kupata usajili kama Hospitali ya Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendelea kuboresha huduma Serikali katika mwaka wa fedha 2016/2017 ilitoa shilingi milioni 250 ambazo zimetumika kumaliza jengo la wagonjwa wa nje ambalo ukamilishaji wake uko hatua za mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuendelea kuboresha miundombinu ya hospitali hiyo ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi. Aidha, Halmashauri kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Siha imeomba wadau mbalimbali ambao wameweza kuchangia jumla ya shilingi milioni 129.38 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya akina mama ambayo iko katika hatua za umaliziaji.
MHE. ESTHER M. MMASI aliuliza:-
Ukosefu wa ajira bado ni changamoto kubwa hasa tunapoangalia takwimu za kidunia na hata katika nchi yetu:-
(a) Je, Serikali imejipangaje katika kulinda ajira za Vijana kupitia Sera ya Ajira?
(b) Kwenye kada ya TEHAMA nchi yetu imekuwa ikipokea nafasi nyingi za ajira kwa Vijana kwenye Taasisi za kifedha kwa kazi nyingi kupelekwa nje ya nchi ikiwemo nchi jirani. Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua changamoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Sera ya Taifa ya Ajira imeweka mikakati ifuatayo katika kulinda ajira za vijana:-.
a) Kuhamasisha mazingira bora ya uwekezaji katika sekta zenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira hususani kilimo, ujenzi, viwanda na biashara;
b) Kuwajengea vijana ujuzi wa fani mbalimbali kupitia programu za ukuzaji ujuzi ili vijana wengi zaidi wapate ujuzi stahiki utakaowawezesha kuwa na sifa za kuajirika, kujiajiri na kuwaajiri wengine;
c) Kusimamia sheria na kanuni za kuwawezesha vijana wazawa wengi zaidi kushiriki katika miradi mikubwa ya maendeleo kama sehemu ya nguvu kazi na watoa huduma; na
d) Utekelezaji wa Sheria ya Uratibu wa Ajira kwa Wageni Na.1 ya Mwaka 2015 ili kulinda nafasi za kazi kwa Watanzania, kwa kuhakikisha Watanzania wanafanya kazi ambazo vinginevyo zingefanywa na wageni.
Mheshimiwa Spika, kada ya TEHAMA ni moja ya Kada ambazo zimewezesha ajira nyingi hapa nchini hivyo Serikali imefanya juhudi kubwa kuhakikisha kunakuwepo naa Wataalam wa kutosha wa sekta hii na kulinda ajira zao kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, moja ni kutoa Wataalam wengi wa fani ya TEHAMA kupitia Vyuo Vikuu na Vyuo vya elimu ya Juu kwa kuhamasisha wanafunzi wengi zaidi kusomea fani za sayansi ikiwemo suala la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, pili ni kuendesha programu za ukuzaji ujuzi ili kuwajengea uwezo Watanzania katika fani ya TEHAMA kupitia mpango wa kitaifa wa kukuza ujuzi na tatu ni kutoa mikopo ya asilimia 100 kwa wanafunzi wa Elimu ya juu kwa Kada ya TEHAMA.
MHE. SHALLY J. RAYMOND (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-

Changamoto kubwa inayowafanya wanawake wa Tanzania wasishiriki kwenye Sekta ya Kilimo na ufinyu wa Bajeti na mitaji kutoka kwenye Taasisi za Kifedha:-

Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya ushiriki wa wanawake kwenye Sekta ya Kilimo ukizingatia changamoto hizo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Kilimo inajumuisha sekta ndogo za kilimo mazao, mifugo, uvuvi na misitu. Bajeti ya Wizara za Sekta ya Kilimo zinajumuisha bajeti ya Wizara za sekta husika, Bodi za mazao na Taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara hizo za Kisekta. Utekelezaji wa bajeti hizo huwawezesha wanaume na wanawake katika shughuli za kilimo. Wanawake wanachangia asilimia 90.4 ya nguvukazi ya wanawake inayotumika katika shughuli za kilimo na huchangia wastani wa asilimia 70 ya mahitaji ya chakula nchini.

Mheshimiwa Spika, katika kutatua changamoto hizo, Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004 kupitia mifuko ya uwezeshaji ikiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake ambao huchangia 4% ya mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kila mwaka. Kwa mfano, katika mwaka 2017/2018, jumla ya shilingi 15,633,312,764.91 zimetolewa kwa vikundi 2,919 vya wanawake na vijana vyenye jumla ya wanawake wajasiriamali 29,190 katika Halmashauri mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa wanawake katika kilimo Serikali, imeilekeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) katika mikopo inayotoa yote isipungue asilimia 20, mikopo hiyo itolewe kwa vikundi vya wanawake na miradi inayoongozwa na akina mama. Hadi Januari, 2019, asilimia 33 ya mikopo iliyotolewa katika vikundi vya wanawake na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ilienda kwa wanawake.

Mheshimiwa Spika, vilevile, benki za NMB na Azania zimeanzisha madirisha maalum ya kutoa mikopo kwa vikundi vinavyojishughulisha na kilimo na miradi mbalimbali. Pia Serikali imehamisisha wanawake kujiunga kwenye vikundi vya ushirika wa akiba na mikopo kama SACCOS, VICOBA ili kupata huduma za kifedha na mikopo kwa urahisi ili kuongeza mitaji yao katika kilimo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeuelekeza Mfuko wa Pembejeo za kilimo kutoa kipaumbele kwa vikundi vya wanawake vinavyoomba mikopo ya kuendeleza kilimo. Vilevile, Serikali imeendelea kutoa hatimiliki za ardhi za kimila na hatimiliki za ardhi za muda mrefu kwa ajili ya kuwawezesha wanawake kumiliki ardhi na kuzitumia hati hizo kama dhamana, kukopa katika Taasisi mbalimbali za kifedha ili waweze kupata mitaji ya kununua pembejeo na zana bora za kilimo ili kuongeza uzalishaji, tija na kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya usindikaji wa mazao kwa kuongeza tija na vipato vyao.
MHE. ESTER M. MMASI aliuliza:-

Mfereji wa Muo Irrigation Scheme (MUU) ni mradi wa Umwagiliaji uliopata fedha takribani Shilingi milioni 248 mnamo mwaka 2018.

Je, kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kukamilisha mradi huu kwa faida ya wakazi wa Old Moshi Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa uendelezaji wa Skimu ya Umwagiliaji Muo kwa ajili ya shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa Old Moshi na Taifa kwa ujumla. Aidha, kwa kuzingatia mahitaji na umuhimu wa uendelezaji wa Skimu ya Umwagiliaji ya Muo Serikali mpaka kufikia mwaka wa fedha 2019/2020 tumeshapeleka jumla ya shilingi milioni 261 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo zilitokana na Mfuko wa Local Government Capital Development Grant jumla ya Shilingi za Kitanzania milioni 51 kwa ajili ya kusakafia mfereji mkuu umbali wa mita 200. Mfuko wa Umwagiliaji wa Wilaya (District Irrigation Development Fund) jumla ya Shilingi za Kitanzania milioni 200 kwa ajili utandikaji wa mabomba kutoka kwenye chanzo cha maji, progamu ya kuendeleza kilimo wilaya jumla ya shilingi milioni 10 kwa ajili ya kuendeleza utandikaji wa mabomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa kazi zifuatazo zilizokwishatekelezwa ni pamoja na ujenzi wa banio kwenye chanzo cha mfereji mkuu umekamilika. Utandikaji na ufungaji wa mabomba class B umbali wa kilometa sita kati ya kilometa nane umekamilika. Ujenzi wa matenki mawili ya kurekebisha msukumo wa maji umekamilika. Ujenzi wa chemba ya kufunika kwenye sehemu ya banio na ujenzi wa mfumo wa hewa katika mabomba umekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Septemba, 2019, Serikali ilituma wataalam wake katika skimu ya Muo kwa lengo la kubaini changamoto zilizopo na kuanisha mikakati na mahitaji ya kuendeleza skimu hiyo. Changamoto zilizobainishwa ni pamoja na kuwepo kwa hitaji jipya la kubadilishwa matumizi ya chanzo cha maji kwa matumizi ya maji ya kunywa badala ya maji ya umwagiliaji na kuwepo ongezeko la shughuli za ujenzi katika skimu hiyo kusababisha kupungua kwa eneo la kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia changamoto hizo Serikali imepanga kuitisha mkutano wa wadau kwa ajili ya kujadili na kupata ufumbuzi wa changamoto hizo. Aidha, baada ya makubaliano ya mkutano wa wadau kuhusu kubadilisha matumizi au la ya chanzo cha maji Serikali itaendelea kutafuta fedha za kibajeti kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya uendelezaji wa skimu hiyo.
MHE. MARIAM D. MZUZURI (k.n.y. MHE. ESTHER M. MMASI) aliuliza:-

Kutokana na kutimizwa kwa masharti na matakwa ya Kisheria ya kutangaza Mkoa wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi ni dhahiri imevutia wadau wengi wa uwekezaji katika nyanja mbalimbali za kiuchumi:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kulinda ajira zisizo rasmi kwa vijana wahitimu Tanzania hasa wa Mkoa wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY PETER MAVUNDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kutangazwa kwa Mkoa wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi, kumevutia uwekezaji katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na za kijamii na hivyo kusababisha ongezeko la ajira rasmi na zisizo rasmi. Katika kulinda ajira za vijana wanaojishughulisha katika sekta isiyo rasmi, ikiwemo Mkoa wa Dodoma, Serikali inatekeleza mikakati ifuatayo:-

Kwanza, ni kuhamasisha vijana wakiwemo wahitimu kuunda makampuni katika Mkoa wa Dodoma, ambapo jumla ya makampuni 12 ya vijana yameundwa.

Pili, kuwezesha vijana kupata mikopo yenye masharti nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Vijana pamoja na mapato ya ndani ya Halamshauri, ambapo katika Mkoa wa Dodoma vijana kupitia vikundi na makampuni 978, wamewezeshwa mitaji yenye thamani ya jumla ya shilingi 2,557,090,486/= kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanzisha au kuendeleza biashara zao.

Tatu, kurasimisha ajira za vijana wanaojishughulisha katika sekta isiyo rasmi kwa kuwatambua na kuwapatia vitambulisho vya mjasiriamali ili kuwawezesha kufanya shughuli zao bila kubughudhiwa.

Nne, kutoa mafunzo ya ufundi stadi katika fani mbalimbali kwa jumla ya vijana 1,240 wa Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kuwawezesha kujiajiri au kuajiriwa katika shughuli za ujenzi na biashara hapa Dodoma kupitia programu mbalimbali.

Tano, kurasimisha ujuzi uliopoatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo katika kada za ufundi mbalimbali kwa vijana 245 wa Mkoa wa Dodoma ili kuwawezesha kujiajiri au kuajiriwa au kuendelea na mafunzo ya ngazi za juu.

Sita, kutoa mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia ya kitalu nyumba (greenhouse) kwa vijana 18,800 nchi nzima, ambapo vijana 800 wanatoka Halmashauri nane za Mkoa wa Dodoma.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-

Serikali imeonesha nia madhubuti kupitia mikakati yake ya kuinua ajira kwa Watanzania.

Je, ni kwa namna gani Serikali imejipanga kuinua ajira kwa vijana kupitia makundi maalum kama vile vijana wa kidato cha nne, darasa la saba na waendesha bodaboda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ili kukuza fursa za ajira kwa vijana kupitia makundi mbalimbali ya ngazi za elimu na waendesha bodaboda, Serikali imejipanga kutekeleza yafuatayo:-

(i) Kuweka mazingira bora ya uwekezaji katika sekta zote zenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira, hususan kilimo na biashara, aidha, katika hili Serikali itajikita zaidi kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji wa viwanda vidogo, vya kati na vikubwa ili kufikia lengo la asilimia 40 ya nguvu kazi nchini kuwa katika sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2020 kupitia Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

(ii) Kuendelea kuimarisha utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambao unalenga kuwasaidia vijana kuweza kujiajiri na kuwapa mikopo ya masharti nafuu na mafunzo ya ujasiriamali.

(iii) Ni kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza Ujuzi nchini ambao umelenga kutoa mafunzo ya vitendo yatakayofanyika maeneo ya kazi ili kuwapa vijana wengi fursa za mafunzo Serikali imeanzisha programu maalum ya kutambua ujuzi uliopatikana nje ya mfumo usio rasmi na kurasimisha kwa kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa wale watakaobainika kuhitaji na kuwapa vyeti. Utaratibu huu unawapa fursa vijana wetu kuendelea na mafunzo rasmi na mfumo rasmi wa mafunzo na pia kutambulika na waajiri au watoa kazi.

(iv) Mwaka 2017 Serikali ilirekebisha Kanuni za Sheria ya Usafirishaji za mwaka 2010 kwa lengo la kuruhusu bodaboda na bajaji kubeba abiria na kurasimisha ajira ya waendesha bodaboda na bajaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa Azimio la Wakuu wa Mikoa la mwezi Novemba, 2014 kuhusu kuongeza fursa za ajira kwa vijana kwa kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na biashara, lakini pia kutoa kipaumbele kwa kununua bidhaa na huduma zinazotolewa na vijana na kutoa mikopo ya masharti nafuu.