Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Katani Ahmadi Katani (1 total)

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwanza naishukuru Serikali yako kwa kuondoa tozo kadhaa kwenye zao la korosho. Swali langu ni je, pamoja na kuondoa tozo hizo, Serikali imeendelea kumnyonya mkulima kwa kukata asilimia 15 ya bei ya soko. Je, Serikali ina mkakati gani kuendelea kumwondolea mkulima tozo hii ambayo ni kubwa sana?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katani, Mbunge wa Tandahimba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Katani pamoja na Wabunge wote wanaotoka mikoa inayolima korosho kwa kazi kubwa waliyoifanya kubainisha matatizo makubwa yanayowapata wananchi wanaolima korosho na hasa wanapolalamikia mfumo ulio bora na imara, lakini kutokana tu na kuwa na tozo nyingi, kama ambazo Mheshimiwa Mbunge amezisema.
Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya maamuzi ya kupunguza tozo zote za hovyo ambazo zilipangwa tu kwa lengo la kutaka kuvuruga mfumo na hatimaye wananchi wakachukia kutumia mfumo ambao unawaletea tija kwenye zao lao la korosho. Hii ni pamoja na tozo za asilimia 15 ambazo zipo miongoni mwa zile tozo, lakini tozo hii ya asilimia 15 kwenye orodha ya zile tozo, ilikuwa iko kwenye eneo la manunuzi ya vifungashio. Vifungashio; kuna magunia ambayo bei yake ni ya juu kidogo, pamoja na nyuzi.
Mheshimiwa Spika, tozo hii sasa itakuwa imeondoka kwa kuwa tumeupa Mfuko unaoitwa Mfuko wa WAKFU, ambao unasimamia maendeleo ya zao la korosho. Mfuko huu umeundwa na wadau wenyewe na unachangiwa na tozo za korosho zinazouzwa nje ya nchi. Inaitwa Export Levy, ambayo inachangiwa kwa asilimia 65 na tozo hii huwa inatozwa na TRA.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mfuko wetu wa WAKFU kwa asilimia zile 65, sasa hivi wana hela nyingi sana kwa ajili ya kukamilisha madhumuni ambayo yamepangwa na wadau ikiwemo na kuhakikisha kwamba, masoko ya zao la korosho yanapatikana. Pili, kuhakikisha kwamba, wananunua pembejeo kwa maana ya mbolea na mbegu, kusimamia uboreshaji wa mbegu hizo na kupanua mashamba ya korosho; pamoja na kugharamia tafiti mbalimbali ambazo zinatakiwa ziwe zinafanywa kwa ajili ya kupata ubora wa zao la korosho.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Katani na Wabunge wote wanaotoka mikoa ya korosho, tozo hii iko sasa kwenye Mfuko wa WAKFU ambao umeingia kwa ajili ya kununulia vifungashio na kwa hiyo, mkulima kwa sasa hana tozo hiyo.