Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Mary Machuche Mwanjelwa (14 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naunga mkono hoja, however, naomba majibu na utatuzi wa tija kwa haya yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ni tatizo hususani katika Mkoa wa Mbeya. Jiji la Mbeya kwa muda mrefu tumekuwa na kilio cha by pass road toka Mlima Nyoka, Uyole, barabara ya zamani kutokea uwanja wa ndege wa Songwe, tumejadiliana kwenye Road Board bila mafanikio. Kwani hii imekuwa ikisababisha foleni isiyopitika kwenye barabara kuu ya Mbeya, barabara kuharibika sana, ajali na vifo vingi kwani malori makubwa yamekuwa yakipita hapo hapo, hii ni hatari kubwa. Nahitaji jibu na ufafanuzi wa kina juu ya hili suala sugu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la barabara ya Dar es Salaam, Tangi Bovu hadi Goba, huu ujenzi umesimama muda mrefu na eneo lililobakia ni dogo sana. Nini tatizo na lini itakamilika kwani itasaidia sana kupunguza foleni nyingine na hii barabara ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Songwe unasuasua sana. Hakuna taa, jengo halijakamilika na ni gate way ya Southern Corridor; ni lini utakamilika kwa ajili ya kupanua wigo wa biashara hii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa ndege wa zamani wa Mbeya umekuwa dumped, umetelekezwa na hauna matumizi yoyote zaidi ya kuvamiwa hovyo, ni nini hatma ya uwanja huu? Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka kitega uchumi hapo au kuipatia Halmashauri ya Jiji, ili paendelezwe?
Mheshimiwa Mwenyekiti, cybercrime imekithiri, ni nini hatma ya hili suala? Mitandao imekuwa inachafua wananchi bila hatua yoyote. Tujulishwe udhibiti wake ukoje? Preventation ni better than cure, kuna wengine wanafahamika waziwazi; nipatiwe majibu ya kina na ufumbuzi kwa haya machache.Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda tu nimshauri Mheshimiwa Waziri ili anapokuja wakati mwingine kwa sababu hii ni bajeti yake ya kwanza ajaribu sana kuangalia yale masuala ambayo ni controversial ili yaweze kuingia kwenye taarifa tusiwe na kuhoji wala kushauri kwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nijikite katika masuala machache sana kutokana na muda wenyewe kuwa mfupi. La kwanza ni katika sekta hii ya utalii ambapo Serikali inapata pato la Taifa asilimia 17.5, ile GDP. Hii ingeweza kuongezeka zaidi lakini inategemea na matatizo ambayo wanayo wale tour operators wetu ambao wako nchi za nje kwa maana ya kwamba ile package wanayochaji pesa za nje zinabaki kule Serikali inapata kiduchu, inaambulia patupu. Naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa atuletee mikakati ambayo itakuwa ina tija ili Serikali iweze kupata pesa nyingi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, hapa Waheshimiwa wengi wanazungumzia suala la concession fee, ni kweli hili jambo Serikali imekuwa ikipoteza fedha nyingi sana na kama tunavyoelewa TANAPA ni shirika kubwa sana na linafanya kazi nzuri sana. Pamoja na hayo, ninachoelewa ni kwamba TANAPA wameshatoa mapendekezo yao kwa ajili ya kuongezea pato Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, lazima tujiulize Waheshimiwa wengi wamesema concession fee imechukuwa muda mrefu hivyo, TANAPA mpaka leo hii, zaidi ya miaka miwili na nusu haina Bodi, masuala mengine hata hili suala la concession fee haliwezi kufanyika bila Bodi ku-approve. Kwa hiyo, pamoja na kwamba suala la Bodi pia Mwenyekiti lazima ateuliwe na Rais, ni jukumu la Mheshimiwa Waziri kama mwenye dhamana kuhakikisha kwamba ana-push TANAPA iweze kuwa na Bodi ili masuala mengine kama haya ya concession fee yaweze kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo katika Shirika hili la TANAPA, Wabunge wengi hapa ndani wamelipongeza. Ni kweli linafanya kazi vizuri, wote ni mashahidi tunajua kabisa kwamba katika programu yao ya CSR, mikoa 16, wilaya zaidi ya 55 zinazopakana na hifadhi wamechangia madawati shilingi bilioni moja, hii ni kazi nzuri. Kama vile haitoshi bado TANAPA ni mojawapo ya mashirika machache ambayo yanachangia gawio kubwa sana kwa Serikali. Mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja katika suala zima la misitu. Waheshimiwa wengi hapa wamechangia, utoaji vibali vya uvunaji ni jipu. Ni jipu kwa sababu hili limekuwa ni tatizo kubwa sana, huko hakujakaa vizuri kabisa, wananchi wanalanguliwa vibali vya uvunaji, vinatolewa kwa kujuana, wanauziana wale wale, vibali hewa. Mheshimiwa Waziri asipokaa vizuri hapa tunamtolea shilingi maana sisi wengine tunatoka katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini. Kwa hiyo, tunataka mkakati wa kina katika suala zima la utoaji wa vibali vya uvunaji na mbinu mbadala tunataka iwepo na yenyewe atuletee majibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema pesa nyingi zinapotea katika sekta hii ya utalii tunamaanisha. Pale Ngorongoro, pamoja na mengineyo, suala zima lile la smart card kwenye gate fees ni tatizo. Naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa atueleze pia suala la smart card kwenye gate fees likoje? Maana vilevile pale kuna utata, pesa nyingi sana inapotea, hili jambo ni very serious na lishughulikiwe mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nije katika migogoro hii ya wakulima, wafugaji pamoja na hifadhi. Kwenye Bunge lililopita nilikuwa katika ile Kamati ya Operesheni Tokomeza Ujangili. Kwa hiyo, ninaposema hivi nina uhakika tulijionea nini katika suala zima la migogoro ya hifadhi, wakulima na wafugaji. Nawashukuru sana Waheshimiwa wengi ambao wamechangia hapa uhifadhi una maana yake, uhifadhi una umuhimu wake katika katika Taifa letu, wakulima wana umuhimu wake na wafugaji wana umuhimu wake, nini kifanyike hapa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wote hapa tumetokana na uhifadhi, tumetokana na wakulima, tumetokana na wafugaji, lakini kila mtu akisimama akaanza kufagilia yale mambo ya kwake hatutafika hata huo uhifadhi pia utakufa. Kwa hiyo, nini kifanyike hapa, Waziri wa Maliasili awasiliane na Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Sheria, Wizara ya Ardhi pamoja na watalaam na watendaji wao, wakae chini, sheria ni msumeno, watuletee masuala ambayo yataleta tija, sheria itumike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kuna wenzangu wengine hapa wameuliza kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili, Bunge lililopita sote ni mashahidi. Baada ya sisi kusoma ile taarifa yetu hapa, Mawaziri wanne wali-step down. Mheshimiwa Rais akaunda Tume ya Majaji mpaka leo hii hatujapata taarifa ili tuweze kujua haki ilitendekaje ama namna gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu ni mchache, naomba niunge mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Jehova kwa kunifanya hivi nilivyo, nayaweza yote katika yeye anitiaye nguvu.)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza kuchangia, nachukua fursa hii kuwashukuru sana wapiga kura wangu wote wanawake wa Mkoa wa Mbeya wa Chama cha Mapinduzi kwa kunichagua kwa kura nyingi sana za kishindo, na mimi nasema sijawaangusha na ninawaahidi sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sera yake nzuri sana ya Hapa Kazi Tu na hakika sasa ni kazi tu. Naomba nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Ardhi na dada yangu Mheshimiwa Angeline pale. Nakumbuka kazi ni nzuri, tulikuwa tunamwombea Mheshimiwa Waziri aifanye kazi hii arudi tena kwenye cabinet na katika Wizara ile ile kutokana na jinsi alivyokuwa ameinyoosha vizuri Wizara hii. Mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Mheshimiwa Waziri, hongera lakini gema likisifiwa sana, tembo hulitia maji. Kaza buti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, naomba niseme tu kwamba Mheshimiwa Waziri tunakupongeza, umetuletea haya makabrasha na timu yako nzima, lakini naomba in future usituletee siku ile ile unayo-present bajeti yako kwa sababu tunahitaji muda tuweze kusoma, kuperuzi na kuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyerere katika concept yake ya uchumi alisema ili tuendelee tunahitaji mambo manne; tunahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Mojawapo ya sifa ya Tanzania tunayojivunia ni ardhi. Ardhi yetu ni kubwa na ni nzuri sana lakini cha kushangaza na cha ajabu ni migogoro isiyokwisha, ni migogoro ambayo kwa kweli ni so much rampant. Nikuchukulia mfano wa kule kwetu Mbeya, kipaumbele chetu sisi Wanambeya ni ardhi; asubuhi, mchana, jioni. Ukiangalia, hii ardhi iko kwenye kilimo, viwanda, elimu, biashara, kila kitu, vyote vinahitaji ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Mnyalu ulikuja Mbeya na umejionea mwenyewe, migogoro ya ardhi iko vibaya sana hususan ule uwanja wa ndege wa zamani. Hata katika maeneo yale yenye makazi holela, ukichukulia pale Iyunga, Mwakibete, Ilemi, Nzovwe, kote na maeneo ya Isanga mbalimbali, ni migogoro mitupu. Nilikuwa naomba ukisimama hapa unapo-wind up utupatie status mpaka sasa hivi maelezo yake ya kina, Serikali katika kuboresha mpango huu ambao ni tatizo sugu kwa Wanambeya imefikia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-declare mimi nilikuwa Mwenyekiti wa hii Kamati, naomba nizungumzie suala zima la Intergrated Land Management Information System. Mheshimiwa Waziri alitupeleka Uganda katika kusomea na kujifunza jambo hili. Wenzetu Uganda wako mbali sana katika suala zima la electronic, hati unaitoa within a day, unaipata siku hiyo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nawashukuru ndugu zetu wa World Bank wameweza kusaidia project hii ambayo mpaka sasa hivi nilikuwa nataka Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wake wa 27 ambapo amezungumzia hili jambo, lakini hajatueleza ni kwa nini hili jambo limechelewa sana mpaka leo hii na lini lita-kick off? Tunataka maelezo ya kina, maana yake tumeambiwa tu project, project; World Bank, World Bank! Mpaka sasa hivi hatujajua nini hatima yake. Tunahitaji maelezo ya kina atakapokuja hapa ku-wind up.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la maeneo ya wazi, maeneo ya Mashamba pori makubwa ambayo yametelekezwa kwa muda mrefu. Nilikuwa nataka kujua nini mkakati wa Serikali katika masuala haya ukizingatia kwamba hata Land Bank hatuna. Land auditing hatujui inafanyikaje! Tunahitaji tunapoelezwa sisi kama Wabunge, tuelezwe maelezo ya kina ambayo sisi hatutakuwa na maswali mengi. Tusiwe tunapigwa blah blah za kisiasa tu hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote, naomba nizungumzie suala zima la mradi ule wa Kigamboni. Huu mradi naomba niseme ni non-start up kwa sababu hii project ambayo tunaizungumzia, pesa inapotea bure tu. Huu mradi ni bora ukavunjwa kabisa, ukarudishwa kwa wananchi wa Kigamboni na Manispaa ya Kigamboni kwa sababu hauna faida. Wizara kwanza ni kubwa sana, resources nyingi zinapotea. Hii Wizara iwe ni eyes on, eyes off; hatuhitaji kwamba iendelee kushikilia mradi wa Kigamboni ambao tayari umeshafeli. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama hapa atueleze mkakati mzima, hii KDC haina haja, wala Wizara isihangaike nayo, huu mradi uvunjwe kabisa urudishwe kwa wananchi kule Kigamboni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba pamoja na Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi...
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba utunze muda wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni sambamba na Tume ya Matumizi Bora ya Ardhi, nimeona wamepewa vote sawa sawa, lakini tukumbuke nini sababu ya kuunda Tume? Tume inapoundwa, lazima kuwe na mpango maalum wa kazi maalum, lakini Tume hii mpaka sasa hivi hatuoni hata umuhimu wa hii wake. Lazima tuseme, ikiwezekana irudi Wizarani ipewe directorate iwe ni kama Idara. Tunahitaji effectiveness ya Tume hii na lazima tunapozungumzia Hapa Kazi Tu, basi tuzungumzie na masuala ya results oriented. Siyo tu kwamba kuna Tume, halafu resources zinapotea bure; na ukizingatia Tume hii imedumu kwa muda mrefu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nahitaji pia Mheshimiwa Waziri atueleze hili suala la zima la D by D ambalo ni muhimu sana, litakuwaje katika Wizara hii ya Ardhi, ukizingatia kwamba D by D na umuhimu wake ukishafikiwa, basi ni utaratibu tu maalum unaotakiwa kufanyika kwa sababu naelewa kuna pros na cons zake katika hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu suala la Shirika la Nyumba. Shirika la Nyumba tunaelewa ni kweli wana management team ambayo ni very much creative na wame-reform kwa sana na shirika lina surplus, lakini Waheshimiwa Wabunge wote hapa ni mashahidi, Watanzania wote ni mashahidi; Shirika hili la Nyumba wakilala, wakiamka wao ni nyumba. Maisha yao siku zote ni nyumba na Watanzania wanaelewa hivyo. Tatizo kubwa, bei yao ya nyumba ni kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo humu ndani tujiulize, ni Watanzania wangapi na wa kawaida ambao ndio asilimia kubwa, wamefaidika na bei ya Shirika la Nyumba? Nasema, viongozi hawa wa Shirika la Nyumba ambao wengi wanatoka kwenye corporate world, wabuni zaidi jinsi ya kupunguza bei...
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Mwanjelwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa fursa nichangie Wizara hii ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninampongeza sana mwanamke wa kwanza katika historia ya Tanzania ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais, mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu. Licha ya kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais mwanamke, lakini vile vile Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amemteua kuwa kwenye jopo la juu kabisa la ushauri jinsi gani ya kuweza kumuwezesha mwanamke. Ninaamini kwa njia hii wanawake wa Tanzania tutanufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo mimi naomba nianze yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni sovereign state, lakini cha ajabu ukiangalia nchi kama Israel, Australia, Uingereza, Canada masuala yote ya viza unapoyahitaji hayapatikani hapa Tanzania. Sasa nilikuwa nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, shemeji yangu, ninayemuheshimu sana, suala la bilateral limefikia hatua gani mpaka visa hazitolewi hapa nchini kwetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala zima la diplomasia ya kiuchumi. Foreign Minister wa Australia by then Julie Bishop aliwahi kusema, just as traditional diplomacy aims for peace and security, so economic diplomacy aims for prosperity. Kwa nini ninasema haya? Hii diplomasia ya kiuchumi ilianza nchini kwetu mwaka 2001, lakini nilikuwa nahitaji sana Mheshimiwa Waziri atuambie, as of to date, sera hii ya kiuchumi imefikiwa vipi na imefanikiwaje na tumei-utilize namna gani kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge Masele pale, maana hii economic diplomacy ndiyo injini ya sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelewa kuna changamoto za pesa, lakini kuna suala zima la commercial attaché, niliwahi kuuliza hapa swali, tatizo la commercial attachés wetu kazi zao hazionekani vizuri na wengine wako inactive ama hawapo kabisa kwenye Balozi zetu. Lakini ajabu nikajibiwa kwamba Wizara hii ni mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapozungumzia economic diplomacy kwa misingi hii sijui ni nini kifanyike. Ushauri wangu kwa Serikali, ni kama huu ufuatao; pamoja na kwamba diplomacy is expensive but in order to move tunatakiwa tufanye nini? La kwanza tunatakiwa tuwe na various capacity building kwa foreign staff wetu ili waweze kujua wanaweza wakaitangaza nchi yetu namna gani kule nchi za nje pamoja na vivutio vyake. Na hawa ndugu zetu ma-foreign staff wanatakiwa pia wawe ma-lobbyists wazuri, wawe negotiators wazuri, wawe smart, waweze ku-strategize waweze kuwa innovative. Na ndiyo maana ninazungumzia tuweze kuwa na capacity building za mara kwa mara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile performance appraisal inatakiwea kufanyika, wapewe marbles, wapewe goals ili tuweze kuwa na deliverables ziweze kuonekana, vinginevyo tutakuwa tunafanya business as usual. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika hizi Balozi zetu tunatakiwa tuwe na tourists experts kama wale wa uhamiaji wanaoshughulikia viza. Lakini hawa tourists experts wetu ambao tunakiwa tuwe nao katika zile Balozi zetu na wenyewe wajaribu kuwa strategists, kwa maana ya kwamba wawe katika zile nchi ambazo tunaweza tukafanya ubalozi wetu na biashara ya utalii kwa vizuri. Kwa mfano, nchi ya China sasa hivi wote ni mashahidi, ni nchi ambayo inakua kwa kasi na vilevile inaweza ikaleta ndege tukawa na uwekezaji; ukizingatia pia Watanzania wengi wanafanya biashara kule China, na vilevile tukaweza kuwa na consulate pale Guangzhou na tukafanya utaratibu wa Watanzania hawa kuweza kuwa na partnership pamoja na wale wenzetu wa China.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni suala zima la shuttle diplomacy. Katika Bunge lililopita jambo hili nililizungumzia sana. Ninatoka Mkoa wa Mbeya, Mkoa wa Mbeya kuna Ziwa Nyasa na tunajua upande wa Ziwa Nyasa kuna suala zima la Heligoland, maana hii ni tangu enzi za Kamuzu Banda. Lakini Mheshimiwa Waziri hapa kwenye taarifa yake hajazungumzia mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa mpaka leo hii imekuwa vipi. Sisi tunaotoka katika Ziwa Nyasa na wenzangu wengine wote tungependa kujua mpaka leo hii suala hili llimefikia wapi na suala zima za shuttle diplomacy limefikia wapi kwa sababu wakati ule Mzee wetu Chissano na wenzake walikuwa wanajaribu kulizungumzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la conference diplomacy. Hii ninajua ina gharama zake na sasa hivi tunajua wengi hawasafiri sana na ndiyo maana nikazungumzia masuala ya foreign staff wapewe ile capacity building, lakini vilevile katika suala zima la bilateral na multilateral basi tujaribu kuangalia sana kama tunaweza tukawa na forums za aina mbalimbali kuweza kufanyika hapa nchini kwetu ili tuweze kuongeza Pato la Taifa, tuweze kutangaza nchi na vivutio vyake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni majengo yetu katika Balozi zetu. Waheshimiwa wengi hapa wamezungumzia, ukweli majengo yetu katika balozi yanatia aibu sana, hakuna fedha. Sasa tufanyeje ili majengo haya yaweze kufanyika katika njia itakayokuwa bora na ya ufanisi? Kwanza yanatakiwa kukarabatiwa; ama tuweze kujenga majengo ya staff wetu, vinginevyo tusipoangalia gharama zitakuwa ni kubwa sana zile za kupangisha. Kwa maana hiyo tujenge balozi zetu, vile vile tuimarishe au tuboreshe makazi ya staff maana na wenyewe wanakuwa hawana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mawazo yangu kwa leo yalikuwa ni machache, nisingependa nigongewe kengele, ninaunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
HE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote ninamshukuru sana Jehova kwa kunifanya hivi nilivyo. Mimi nitachangia katika maeneo mawili tu kwa leo, katika eneo la uchukuzi pamoja na ujenzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijamtendea haki Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, jemedari wetu na mtumishi wa Mungu huyu Dkt. John Pombe Magufuli kwa mara ya kwanza kabisa katika historia ya Tanzania tumeweza kuwa na flyovers Dar es Salaam na tutakuwa nayo, lakini pia Serikali imeweza kujenga standard gauge kwa upande wa reli ya kati. Ninaamini sasa na reli yetu ya TAZARA itaangaliwa upya ili iweze kuboreshwa zaidi kutokana na umuhimu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Ndege la Taifa (ATCL). Sasa hivi tumeweza kuwa na national carrier yetu, ni jambo jema na shirika hili limefufuliwa. Napenda kutia mkazo kwa Waheshimiwa Wabunge ambao wamesema kabisa kwamba mashirika haya ambayo yako chini ya Wizara hii, yaweze kupewa full autonomy ili yajiendeshe kibiashara, kwa maana ya kwamba yasiingiliwe ili marketing teams zao ziwe na ubunifu zaidi. Kana kwamba hiyo haitoshi wajaribu kuangalia ni jinsi gani wanaweza wakawa wabunifu kimkakati zaidi kujaribu kwenda katika nchi ambazo zitakuwa zinatuletea mapato mengi zaidi kwa kuongoza utalii wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niende kwetu sasa kule katika uwanja wa kimataifa wa Songwe pale Mbeya. Katika ukurasa wa 169 tumeona Serikali imetenga milioni 1,530 kumalizia jengo na mambo mengine, lakini mimi nilikuwa ninaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa ku-wind up atueleze suala zima la taa za uwanja huo wa ndege wa Songwe kutokana na umuhimu wake. Kuna ndege mara kwa mara zimeshindwa kutua, wewe mwenyewe ni shahidi kutokana na kwamba uwanja huo hauna taa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba pesa ya dharura iweze kutolewa ili uwanja wa ndege wa Songwe tuweze kupata taa wakati wowote wananchi waweze kufurahia huduma hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia naamini wote watasema na Mheshimiwa Waziri anaelewa pale kwamba siwezi kukaa chini bila kuzungumzia barabara ya by-pass, barabara ya mchepuko kutoka Uyole hadi uwanja wa ndege wa kimataifa wa Songwe, na jambo la kusikitisha sijaona hata kwenye kitaba cha taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa, sijaona commitment ya Serikali. Hili jambo ni kizungumkuti, nimekuwa nikilipigia kelele mpaka Waziri aliyepita wa Ujenzi ambaye ni Rais wetu mpendwa sasa hivi, hili jambo analijua na alishatuahidi. Vilevile kana kwamba haitoshi mpaka kwenye vikao vyetu vya Road Board vya Mkoa tulishakubaliana kwa pamoja, tatizo ni nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri atueleze hapa wana Mbeya tusikie, kwa sababu foleni msongamano kutokea Uyole mpaka Mafiati pale barabara haipitiki kabisa, dakika 10 inachukuwa saa tatu. Mimi bila kusita Mheshimiwa Waziri kaka yangu ninaekupenda na kukuheshimu sana nitashika shilingi mpaka kieleweke, maana hili jambo sasa hatuelewi sisi Wana-Mbeya.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini barabara hii ya mchepuko madhara yake ni mengi, inaleta ajali, inaharibu barabara. Vilevile itakapokuwa ina mchepuko sisi wana Mbeya kwetu ni faida kwa sababu tunaweza tukawa pia tuna bandari kavu. Ninayoyazungumzia ni haya malori
makubwa katika hii barabara ya mchepuko, sijazungumzia magari madogo; kwa hiyo Mheshimiwa Waziri anaelewa na alishakuja Mbeya na tumezungumza sana hili jambo lifike muafaka na lifike mwisho, maana mambo haya ya upembuzi yakinifu hata Mheshimiwa Rais hataki kuyasikia, tunataka utekelezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabla sijakaa ni barabara ile ya Isyonje – Mbeya Vijijini hadi Makete kupitia Kitulo, hii barabara inaunganisha mikoa miwili. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri atueleze, kwa sababu kule kuna Hospitali ya Mission ya Ikonda ambayo inasaidia wananchi wengi sana, actually wananchi wote wa Mikoa ya Nyanda za juu Kusini.
Kwa hiyo, nilikuwa ninaomba barabara ya kuunganisha mkoa wa Mbeya na mkoa wa Njombe kwa maana ya kwamba Makete kupitia Kitulo kwa ajili ya wananchi wetu hawa wanokweda kwa wingi kuhudumiwa pale Ikonda basi Mheshimiwa Waziri atuletee majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache ninaomba kuunga mkono hoja bajeti hii, ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naunga mkono hoja hii ya Wizara husika. Naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Jemedari Mtukufu Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli na wasaidizi wake wote. Kubwa la msingi tuwaombee mema kwa Mungu. Hata hivyo nina haya machache ya kutaka ufafanuzi na ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inasomesha Madaktari wengi kwa gharama kubwa sana: Je, ina mkakati gani wa kuwa-retain angalau kuwa na mkataba wa win win situation kwani kuna uhaba sana wa Madaktari kutokana na wengine kukimbilia nchi za nje for green pastures? Uzalendo kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya ya mama na mtoto inaelekea mwaka huu vifo vimeongezeka. Kutokana na data ambazo zinaeleweka, nini chanzo na mkakati wa kuboresha? Tukumbuke mama ndiye familia. Elimu kwa umma iongezwe kuhusu umuhimu wa kujifungulia hospitali au zahanati. Pia akinamama wengi hawana uwezo, hivyo ni muhimu pia kuwapatia tools za wakati wa kujifungua endapo kutakuwa na dharura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ina-extend wodi ya watoto kwa juhudi binafsi na ubunifu. Nampongeza sana Mkurugenzi wa Hospitali hiyo Dkt. Mbwanji. Hata hivyo, nahitaji kujua contribution ya Serikali katika ujenzi huo, kwani Hospitali hii ndiyo inayotoa huduma kwa Mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini na kwingineko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimba na ndoa za utotoni ni tatizo sugu nchini kwetu, kwani licha ya kuwakatisha masomo watoto wa kike, pia inawaathiri kiafya na kisaikolojia. Hili suala kwa kiwango kikubwa linatokana na mila potofu na imani nyingine za dini ambapo sasa Serikali ichukue hatua na jitihada za ziada kwa kuzidi kutoa elimu kwa umma, kukutana na wadau husika, mfano makundi ya dini, Machifu na Serikali. Kwa Wizara husika, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wizara ya Katiba na Sheria ilete Muswada wa kubadilisha Sheria hii ya Ndoa na Mimba za Utotoni. Nashauri umri uongezwe toka miaka 14 iwe 18 na hatua kali zichukuliwe kwa wahusika wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nahitaji kujua why TACAIDS (PM‘s Office); at the same time, why NACP (Ofisi ya Wizara ya Afya office)? Maana wote wanashughulikia masuala ya UKIMWI; huu ni mwingiliano/mgongano wa majukumu na kupoteza fedha za walipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Azimio la Abuja la asilimia 15 limeshakamilishwa kwa hapa nchini kwetu? MDG’s/SDG’s limefanikiwaje kuhusu yale malengo yake hapa nchini kwetu? Mpango wa Afya ya Msingi (MAM) tunahitaji tupewe data; Serikali imefikia wapi? Kwani hii iko katika Ilani yetu ya Uchaguzi wa CCM na huduma bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika Wizara hii muhimu sana ya Viwanda na Biashara. Mimi kama mama na mzazi naomba nichukue fursa hii kuwapa pole familia zote za wale vijana wetu waliofariki pale Karatu, zaidi ya 33 na Mwenyezi Mungu aziweke roho zao mahali pema, peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Komandoo, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa Kauli Mbiu yake mahiri kabisa ya kwamba ‘Tanzania ya Viwanda Inawezekana’. Amekuja na good spirit ya uchumi wa viwanda na nina hakika kabisa tukimuunga mkono kwa vitendo inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natoka katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na naelewa kabisa kwamba Serikali haijengi viwanda, Serikali ina-facilitate viwanda. Hata hivyo, pamoja na hayo nataka kujua, Serikali inapoingia katika miradi ya kimkakati kama vile Liganga na Mchuchuma, nime- declare interest mimi natoka mikoa ya huko, lakini Serikali hii haitoi GN (Government Notice).

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo yake ni kwamba, miradi mingi inasimama. Haijulikani miradi hii itaanza lini? Miundombinu haieleweki, Power Purchase Agreement zake hazieleweki. Namwomba kaka yangu Mheshimiwa Mwijage pamoja na kujieleza vizuri sana, lakini atuletee majibu yenye tija atakapokuja ku-wind up hapa juu ya suala zima la Mradi ule wa Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala zima la kodi. Kodi za VAT kwa wawekezaji wenye viwanda nchini ni tatizo kubwa sana. Wawekezaji hawa wanachajiwa VAT kwenye utengenezaji wa bidhaa za ndani, lakini cha ajabu na cha kusikitisha sana ambacho ambacho nashindwa kuelewa mpaka kesho, bidhaa hizi zinazokuwa imported kutoka nje hazina VAT. Sasa nashindwa kuelewa kabisa hapa, hivi tunauwa hili soko la ndani ama tunajenga? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ni kwenye hizi textile factories, hata hapa Dodoma kwenyewe kuna kiwanda cha gypsum mpaka kimefungwa kwa sababu hozohizo ambazo mimi ninazitoa. Naamini inawezekana kabisa buy Tanzania use Tanzania, tujivunie products zetu za hapa nchini jamani, inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la hii NEDF (National Enterprenuers Development Fund). Hii pesa Serikali inahitaji iipe Wizara kwa nguvu sana kwa sababu, inasaidia sana kuinua wafanyabiashara wadogo wadogo. Hivyo tunaomba Serikali itilie mkazo suala zima hili la NEDF na hii itasaidia kuleta kile kitu tunaita One District One Product, kwa sababu yote haya yanawezekana tukiwa na mikakati thabiti na yenye tija kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na haya yote mwenzangu pale Mbunge wa Muheza, Mheshimiwa Balozi Adadi amezungumza. Tunazungumzia ukuaji wa viwanda, mimi natoka Mbeya, kule kwetu Mbeya kuna viwanda vingi sana vimekufa yamebaki ni magofu tu. Tunaelewa kabisa ufufuaji wa viwanda uko chini ya TR, lakini pamoja na hayo tunataka Serikali itupe mkakati wa ufufuaji wa viwanda hivi umefikia wapi kwa sababu kule kwetu Mbeya majengo yale yamebaki ni magofu, rasilimali zinapotea bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya yote ni suala ambalo halieleweki, tunahitaji Mheshimiwa Waziri hata kama iko chini ya TR tuletee mkakati mzima wa Serikali juu ya ufufuaji wa viwanda ili twende na dhana nzima ile inayosema ukuaji wa viwanda, ufufuaji wa viwanda na ujengaji wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengine ninayozungumza kule kwetu Mbeya Textile ni magofu, Tanganyika Packers magofu, Sijui kutengeneza sabuni vyote hivyo ni magofu, ni magofu, ni magofu! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwenyewe unaelewa, hii ni hasara; hata zana za kilimo; ni hasara kubwa. Rasilimali zetu zinapopotea bure ina maana Serikali yetu hii yenye nia njema ya Awamu ya Tano tunakuwa hatufikii zile ndoto zetu tunazosema ukuaji wa viwanda. Kama ikishindikana worse to worse pia tupate PPP, provided tunaweza kupata ile win win Situation. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nisigongewe kengele, naunga mkono hoja hii ya Biashara na Viwanda, lakini kaka yangu Mheshimiwa Mwijage akija hapa atuletee majibu ambayo yana tija kwa vitendo. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naunga mkono hoja ya bajeti ya Wizara hii. Pamoja na hayo pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuweka kipaumbele cha maji kwa kuzingatia pia kuwa ipo katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maji, Mheshimiwa Injinia Lwenge, Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Injinia Kamwelwe pamoja na timu nzima ya Wizara hiyo kwa uzinduzi wa miradi mikubwa ya maji ya Ziwa Viktoria na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, maji ni uhai, bila maji hakuna maisha. Huduma ya maji mijini imekuwa ni tatizo. Kwa mfano, kule Jijini Mbeya maji hukatika mara kwa mara na kuletewa bili kubwa ya maji na nina uhakika hili ni tatizo katika miji mingi tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 71, unazungumzia kuhusu uboreshaji huduma ya maji katika Jiji la Dar es Salaam, hili limekuwa ni tatizo la muda mrefu. Kwanza sewage system yake ni mbovu sana katika jiji lote hususan mvua ikinyesha na hivyo kusababisha uharibifu wa mazingira na magonjwa ya mlipuko. Katika eneo la Mbezi Beach Juu kuelekea Hospitali ya Masana–Goba Road, maji yamekuwa hakuna kwa miaka mingi na hakuna dalili ya ufumbuzi wa tatizo hili, zaidi tu ya wananchi kupigwa danadana kuwa kuna bomba la mradi wa Wachina. Wananchi wamekuwa wakinunua maji kwa gharama kubwa kwa miaka mingi sana bila suluhisho wala ufumbuzi wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbeya Jiji kulikuwa na mradi mkubwa sana uliozinduliwa kwa msaada wa Serikali ya Ujerumani (KFW) lakini hadi leo maji yanakatika hovyo na bila taarifa yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nahitaji kujua Serikali ina mkakati gani katika suala zima la Mfuko wa Maji. Mfuko huu utasaidia sana kutatua kero nyingi zisizo za lazima kimkakati mijini na vijijini. Mfuko huu unatakiwa uwe mkubwa kibajeti ili kuboresha huduma ya maji nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Awali ya yote naomba niwatakie Waislam wote nchini na duniani kote Ramadhan Kareem. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais, Jemedari wetu kwa tendo lake la kihistoria na la kizalendo kabisa juu ya suala zima la mchanga wa dhahabu unaojulikana kama makinikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba mikataba mibovu na kukosa uzalendo ndivyo vilivyotufikisha hapa tulipo, wala siyo siri. Pamoja na hayo, hii ni vita yetu sote Watanzania, kama Mheshimiwa Lema alivyozungumza, Mama Mheshimiwa Profesa Tibaijuka naye amezungumza masuala ya UNCTAD, lakini lazima tumuunge mkono Mheshimiwa Rais wetu. Hii vita ni yetu sote kwa vizazi na vizazi vijavyo, kwa sababu vita hii aliyoanzisha Mheshimiwa Rais ni vita ya uhuru wa nidhamu na uchumi katika masuala mazima ya kidiplomasia ya uchumi. Nina uhakika hata Mheshimiwa Waziri husika naye ataliweka hili jambo kidiplomasia zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka kuzungumzia kwa uharaka sana ni suala zima la commercial attaches wetu katika Balozi. Nimekuwa nikisema hili kwa muda mrefu sana, kuwa Mabalozi wetu na commercial attaches wetu kwa diplomasia ya kiuchumi ambayo imeanza tangu mwaka 2001, tunahitaji Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up atueleze performance targets zao kama wanapewa ama hawapewi kwa maana ya kwamba, je, wanapewa marbles? Vilevile mid reviews zinafanyika ama hazifanyiki? Tunaomba hilo tuweze kuelezwa kama wanafanya kazi kimkakati, basi tunahitaji wawe kimasoko zaidi na matokeo chanya tuweze kuyaona. Vinginevyo ikishindikana nitashika shilingi ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 18 mpaka 50 amezungumzia conference diplomacy, tunampongeza, matokeo chanya tumeyaona, sihitaji kwenda kwa urefu na mapana ni viongozi gani ambao wameweza wakijadiliana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala zima la shuttle diplomacy. Mimi natoka katika Mkoa wa Mbeya, kuna Ziwa Nyasa ambalo mgogoro wake ni wa muda mrefu sana. Hii shuttle diplomacy kama imeshindikana, worse to worse basi tuingie katika sanctions kama ambavyo iko kule katika nchi ya Burundi. Shuttle diplomacy naona haifanyi kazi inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijakaa, naomba niipongeze Serikali kwa kufungua Balozi mbalimbali pamoja na Ubalozi wa Israel. Nimekuwa nikilia kwa muda mrefu sana lakini nikasema pia wengine kule sisi ni Taifa teule, ndiko tunakokwenda kuhiji na pia kama nchi mengi tunajifunza kutoka kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu ni mfupi, naunga mkono hoja, nakushukuru. Ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa ufupi sana nataka nizungumzie juu ya korosho zetu, hakika ni zao bora mojawapo la kimkakati, ambalo Serikali imewekeza na linafanya vizuri sana katika kumkomboa mkulima pamoja na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hivi karibuni kulikuwa na allegations za mawe kuwepo katika magunia ya korosho kule Vietnam. Sisi kama Serikali hatujakaa kimya tumejipanga na kama Serikali pia tumeunda timu na tumewapa wiki mbili na tutapata majibu na wote watakaobainika tutawachukulia hatua kali na za kisheria na tuweze kujua adui yetu ni wa ndani ama ni wa nje. Kwa sababu hili ni suala la uhujumu uchumi, naomba niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba kama Serikali tunahakikisha kabisa kwamba zao la korosho ambalo ni zao mojawapo bora tunafika kiwango cha juu na tutakuwa katika ramani ya dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala zima la Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Kilimo. Naomba niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba sisi kama Serikali tumejipanga kuhakikisha kwamba tunaandaa Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Kilimo (ASDP II) na Waheshimiwa wote tutawaalika kwenye uzinduzi wa Mpango Mkakati huo wa Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba niseme kabisa kwamba ninaunga mkono hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninamshukuru sana Jehova kwa kunifanya hivi nilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili kwa sababu hii ni mara yangu ya kwanza kwenye hotuba hii, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mbeba maono wa Taifa hili, kwa imani yake kwangu na kuniteua ili nihudumu kwenye Serikali yake ya Awamu ya Tano katika nafasi ya Naibu Waziri, Wizara ya Kilimo. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Rais kuwa naendelea kumuomba Mungu azidi kunipa macho ya rohoni na kamwe nisimuangushe yeye na Taifa letu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa napenda niwashukuru ndugu na wanafamilia yangu, hususani watoto wangu, marafiki zangu wapendwa Joseph and David kwa kuniombea na watumishi wa Mungu wote kuniinua mbele za Bwana katika kutekeleza majukumu yangu haya mapya. Aidha, napenda kuwashukuru wapiga kura wangu, Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mbeya ambao wapo mahali hapa ukumbini na ninapenda kuwathibitishia kuwa ni ahsante, tuko pamoja na A luta continua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru Waziri wangu Mheshimiwa Engineer Dkt. Charles Tizeba, Mbunge, kwa ushirikiano na miongozo anayonipa katika kutimiza majukumu yangu kwenye utumishi wangu wa kila siku kama Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuwashukuru watendaji Wakuu wa Wizara Engineer Mathew Mtigumwe - Katibu Mkuu Kilimo; Dkt. Thomas Kashililah, Naibu Katibu Mkuu, Watendaji wote katika Wizara, Taasisi na Mashirika yaliyo chini ya Wizara kwa ushirikiano wao katika kufanikisha uwasilishaji wa hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nikushukuru wewe na Wabunge wenzangu wote kwa ushirikiano na ushauri mwema ambao mmekuwa mkinipa na kunitia moyo, pia bila kumsahau Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, Mungu awabariki nyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia hoja kwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizochangiwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza naomba nitoe ufafanuzi wa baadhi ya Wabunge kuhusu TANECU. Kama inavyofahamika kwamba TANECU ina vyama vya ushirika vya mazao kwa maana ya AMCOS vipatavyo 186 vinavyojumuisha AMCOS za Wilaya ya Newala na Tandahimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilieleze Bunge lako tukufu kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara Wilaya na nilipata maombi ya kuigawa TANECU kutokana na ukubwa wa chama hicho. Aidha, msingi mwingine wa kuigawa TANECU ni ukweli kuwa viongozi wa chama hicho walihusishwa na ubadhilifu na uzembe. Hali hiyo ilibainika pia baada ya uchunguzi uliokuwa umefanywa na tume iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo Serikali kuanzia leo inaagiza kuwa Chama Kikuu cha TANECU kigawanywe ili kukinusuru chama hicho na pia katika kuimarisha ushirika. Kutokana na hatua hiyo Newala itabaki kuwa na AMCOS 53 na Tandahimba itakuwa na AMCOS 133 na Serikali inasisitiza kabisa kwamba utekelezaji wa maamuzi haya ufanyike kabla ya msimu huu kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali inatoa maelekezo kwa Wakuu wa Wilaya wote nchini na Wakuu wa Mikoa wote nchini kwa kushirikiana na Maafisa Ushirika wa Wilaya na Warajisi Wasaidizi wa Mikoa kusimamia mwenendo wa ushirika kwa ukaribu na kuwa ikidhihirika kuwepo uzembe wa aina yoyote katika utekelezaji wa maagizo hayo basi hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao. Ikumbuke kabisa kuwa kwamba katika utelezaji wa suala hilo Serikali haipo tayari kabisa kulipa madeni yoyote ya nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili naomba nifafanue hoja chache za Kamati na mengine Waziri wangu atayatolea ufafanuzi kwa mapana.

Katika hizo hoja za Kamati walisema kwamba hakuna bajeti ya maendeleo iliyotengwa kwa Tume ya Maendeleo ya Ushirika. Naomba niwaeleze Wabunge wenzangu kwamba baada ya kukamilika kwa programu ya mageuzi na modernization ya ushirika ile ya mwaka 2015 kwa maana ya Cooperative Reform and Modernization Program, Wizara imekuwa ikiandaa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) ambapo kuna miradi kadhaa ya kuendeleza ushirika ambayo itaratibiwa na kusimamiwa na tume ya maendeleo ya ushirika lile Fungu 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara inaiongoza Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuandika maandiko mapya ya miradi na kuyasajili katika Wizara ya Fedha na Mipango. Kuanzia mwaka ule wa 2019/2020 tunatarajia Tume hii ya Maendeleo itaweza kujisimamia yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, Kamati imeshauri Serikali kuchukua hatua kwa mawakala waothibitika kuwa ni wadanganyifu pamoja na maafisa wa Serikali walioshiriki kwenye udanganyifu huu. Naomba nilieleze Bunge lako tukufu kwamba katika zile hatua za awali watumishi wa Serikali wote waliohusika wameshakamatwa pamoja na vile vyombo vya dola vimeshawakamata na wamechukuliwa hatua kali sana. Kuhusu mawakala hawa uhakiki unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo Kamati imeishauri ni kwamba ni vyema midada ya zao la kahawa ikaongeza ili kuwa na wigo wa kutosha na hivyo kuwezesha upatikaji wa soko la uhakika. Naomba nilieleze Bunge lako tukufu kwamba kwa sasa minada ya kahawa inafanyika mara moja kwa wiki Mjini Moshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kahawa ikishakuwa tayari kwa mauzo katika maeneo ya uzalishaji nchini hutoa sampuli na kupelekwa Moshi kwa ajili ya mauzo kwa ushindani. Suala la kuongeza minada halileti tija kwa kuwa litaongeza gharama za uendeshaji na kupunguza ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nimeongea kwa ufupi sana ili nisigongewe kengele, lakini Mheshimiwa Waziri wangu ataeleza kwa mapana na marefu na naomba niseme tena, naunga mkono hoja, ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue fursa hii kukushukuru wewe binafsi, lakini kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza na ni bajeti yangu ya kwanza, nimshukuru sana Jehova, lakini nimshukuru Mheshimiwa Rais pia kwa kuendelea kuniamini na kunipa nafasi hii nimsaidie kwenye eneo hili. Nimshukuru pia Waziri wangu, Mheshimiwa Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika, kwa kunipa ushirikiano mzuri na vilevile kunipa mwongozo mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajibu kwa ufupi, lakini nichukue fursa hii pia kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia kwa mdomo na vilevile wale waliochangia kwa maandishi katika hotuba yetu au bajeti ya ofisi yetu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Vilevile niishukuru Kamati yetu ya Bunge na niombe tu kusema kwamba yale yote ambayo yamechangiwa kwa maandishi, kwa mdomo tumeyapokea tumeyachukua na tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi kabisa kama nilivyosema nitayajibu kwa pamoja nikianza na lile la kukaimu. Leo asubuhi nimejibu hapa suala hilohilo la kukaimu kwamba kuna watumishi wengi, kuna viongozi wengi wanakaimu kwa muda mrefu. Ukweli ni kwamba wamekuwa wakikaimu kwa muda mrefu kutokana na kwamba hizi nafasi huwa wanakaimishwa kule na waajiri wao kienyeji tu, unakuta kwamba huyu anampenda basi anaona ni bora akakaimu kwenye hiyo nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba, kuna waraka kabisa umetumwa mwaka jana Septemba, 2018 kwamba nafasi zote zile za kukaimu lazima zipate kibali kutoka Utumishi na kukaimu kwenyewe kusizidi miezi sita. Kukaimu ni nafasi ya muda, sio kwamba maana yake wewe utathibitishwa au tayari umeshateuliwa, hapana. Kwa hiyo niwatake waajiri wote nchini kuhakikisha kwamba wanafuata sheria, kanuni na taratibu wanapokuwa wanakaimisha wale viongozi kule katika maeneo yao ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kwa ufupi ni kuhusu watendaji wakuu kuhamahama na watumishi kwenda kwenye ofisi zao nyingine. Naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba watendaji wakuu kuhama na watumishi hiyo sio sahihi kwa sababu utumishi wa umma ni obedience, utumishi wa umma ni utii, kokote kule unakokwenda, kwanza ukipewa transfer unatakiwa kufanya kazi mahali popote utakapokuwa umepangiwa, lakini vilevile na kule unakokwenda na kwenyewe kuna watumishi wa umma. Kwa hiyo sio vizuri kusema kwamba unahamahama na watumishi, utawakuta kule na wao sana sana unachotakiwa kufanya ni kuwajengea uwezo ili na wenyewe waweze kuwa ni watendaji wazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu muda wa likizo ya uzazi; naomba niseme mimi pia ni mama, tunaelewa adha ya kujifungua. Likizo ya uzazi, naomba niseme, sisi kama Serikali katika zile siku 84 tumeongeza siku 14 zaidi, lakini tunaelewa kama wanawake consequences za kujifungua mtoto zaidi ya mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine lililozungumzwa ni idadi ya wanawake ile 50 kwa 50. Katika utumishi wa umma, naomba niseme kinachoangaliwa ni sifa, vigezo, ubunifu na umahiri wako wa kazi na vilevile je, unaendana na ubunifu na kasi ya Serikali tuliyopo, sio tu kwamba eti kigezo chako kitakuwa kwa vile ni wewe ni mwanamke, kuwa mwanamke ni sifa ya ziada endapo kuna maeneo mawili labda umechuana na mwanaume lakini sasa wewe kwa sababu ni mwanamke basi hapo unapewa priority.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ndugu zangu wanawake sote tunaelewa sisi ni jeshi kubwa, tuendelee kujiamini, tunaweza tukipewa, kubwa la msingi na sisi tunapobebwa tuoneshe kwamba tunabebeka. Hili sizungumzii masuala ya Madiwani na Wabunge, nazungumzia katika utendaji kazi kwenye utumishi wa umma na wanawake ni jeshi kubwa. Kwa hiyo tukibebwa lazima tuoneshe tunabebeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kutowapandisha watumishi mishahara. Hili suala lilikuwa limesitishwa kutokana na sababu mbalimbali, lakini sisi kama Utumishi, naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba vijana wetu wa kizalendo, vijana wetu wa Kitanzania tumekuwa tukitumia ule Mfumo wa Lawson, Version 9, lakini sasa hivi hawa vijana wetu wa Kitanzania wanaleta mfumo mwingine mpya ambao una nguvu zaidi, capacity yake ni kubwa zaidi na gharama zake ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mfumo tutaanza kuutumia kuanzia Juni na naomba niseme katika mfumo huu tutakuwa tumeboresha mambo mengi sana; masuala kwa mfano yale ya OPRAS, utendaji kazi Serikalini, watu wamekuwa wakifanya kazi kimazoea. Kwa hiyo ule Mfumo wa OPRAS ambao tutakuwa tumeuanzisha kutokana na mfumo wetu huu, wenyewe utasaidia kuziba mianya ya upendeleo, lakini vilevile kuziba mianya ya chuki, kwamba mwingine kwa vile anampenda fulani basi anamwongeza cheo au mwingine kwa sababu hujamsalimia asubuhi basi hakupendekezi. Kwa hiyo mfumo huu utakuwa ni wa kuongeza ufanisi katika utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa kwenye mfumo huu pia tunatarajia kuanzisha One Stop Centre katika maeneo yote ambayo yanatolewa huduma na utumishi wa umma. Tunategemea kuanzisha One Stop Center ili kusiwe na Mtanzania yeyote, mwananchi yeyote wa Kitanzania ambaye yuko katika Serikali ya uadilifu ya Awamu ya Tano kwamba asafiri kutoka Kigoma mpaka kwenda Mwanza, kwa hiyo One Stop Center kupitia mfumo huu itakuwa imeanzishwa katika mkoa mmoja na huduma zote atakuwa anazipata mahali pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie suala la utumishi wa umma; michango mingi imetoka hapa na sote tunaelewa kwamba Chuo cha Utumishi wa Umma ni chuo nyeti na naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba watumishi wa umma wote wanaoajiriwa kwa mara ya kwanza, nitoe rai, hata kwa waajiri, wote nchini kuhakikisha kwamba wanapitia kwenye Chuo chetu cha Utumishi wa Umma, hii ni mandatory wala sio ombi na wale wote ambao watakiuka maagizo haya watachukuliwa hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu unapopita kwenye Chuo cha Utumishi wa Umma kule kuna mambo mengi ambayo inabidi tufundishwe; jinsi gani ya kutunza siri za Serikali, jinsi gani ya kuwa na uadilifu, jinsi gani ya kuwa na uzalendo na mambo kama hayo. Kwa hiyo naomba nitoe rai kwa waajiri wote nchini kuhakikisha wale wote wanaoajiriwa wanapita kwenye Chuo cha Utumishi wa Umma ili kupikwa kama watumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja na ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2017.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie hoja hii ya Finance Bill. Awali ya yote, naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri, Muswada wa Sheria ya Fedha ni vema ukaletwa Bungeni siku ile wakati Waziri wa Fedha na Mipango anaposoma bajeti kuu kwa sababu na huu ni Muswada kama Miswada mingine tofauti tu ni kwamba huu ni Muswada wa Bajeti Kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba niipongeze sana Serikali kwa bajeti nzuri sana na kwa Muswada mzuri sana, Muswada huu ni kwa Watanzania na kwa manufaa ya Watanzania. Nikisema hivyo nina mifano michache kabisa kwamba Serikali hii sikivu sasa imeweza kuwa na zero rate kwenye auxiliary services, imeweza kuondoa exemption kwenye capital goods kwenye zile sekta ambazo ni za kimikakati zaidi, imeweza pia kutuondolea motor vehicle license, imeweza kuondoa SDL kwenye mashule binafsi na mengi kwa kusikiliza kilio cha Watanzania kwa manufaa ya Watanzania. Nawapongeza sana sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kwamba, tuko katika sera ya viwanda na uchumi kwa Awamu yetu hii ya Tano, sasa jambo la kwanza ambalo tunatakiwa ni ku- promote viwanda vyetu na bidhaa zetu za ndani bila kuzididimiza na jambo la msingi ni kuziangalia na kuziboresha zaidi, kwa viwango ili tusiweze kudidimiza bidhaa zetu hizi za ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu, viwanda vya vinywaji baridi, Serikali ilitaka kuongeza excise duty pale ya five percent na wao wakaomba isiwekwe, wakakubaliwa wakapata relief, waka-expand wakaongeza ajira. Mfano kule kwetu Mbeya kuna Pepsi, Coca-Cola na kadhalika, hivyo Serikali ikapata faida zaidi. The more relief the better for the economy wote tunaelewa hilo, vilevile ajira imeongezeka, bei inakuwa siyo kubwa, uchumi pia una– expand, pia kuna kuwa na value chain nzuri na vilevile inakuwa pana hata kwa akinamama lishe, kwa Machinga, na kadhalika, hiyo yote ni kwamba wasipoongeza hii kodi kwani pia hata ile corporate tax pamoja income tax pia vyote vinakuwa juu kwa pande zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kwa wale wenye viwanda vikubwa, wanaotumia sukari ya viwandani, waliwekewa utaratibu wa kutozwa bond ile ya asilimia 15, hadi Serikali itakapotathmini matumizi sahihi ndiyo warejeshewe hiyo pesa. Cha ajabu pesa hii hairejeshwi.

Tunaambiwa Escrow Account, basi iweze kufunguliwa kwa haraka sana, kwa sababu mpaka dakika hii tunaongea kuna bilioni 20 za wafanyabiashara hazijareshwa kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, naamini sasa masuala ya uingizaji sukari yamekwisha, udhibiti wa mianya pia umeongezeka katika Awamu hii ya Tano, kwa hiyo hakuna longolongo. Kwa maana hiyo, naamini yote hayo yatafanyika na wafanyabiashara hawa naamini Escrow Account ikifunguliwa watarudishiwa fedha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, kwa kweli Mheshimiwa Dkt. Mpango wa Mipango pamoja na timu yako nzima na Serikali sikivu, mmesikia kilio cha Watanzania, hii ni bajeti ya mfano kwa mara ya kwanza. Kama nilivyotoka kuzungumza katika opening remarks yangu, Watanzania wote huko mitaani wamefurahishwa na bajeti hii na kila mtu anashangilia wala siyo siri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote mazuri naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Serikali Mtandao wa Mwaka 2019
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Naibu
Spika, nianze kipekee kwa kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote mliochangia kwa kuongea vilevile kwa maandishi Muswada wa Sheria ya Serikali Mtandao wa mwaka 2019 na kwa maoni na ushauri wenu mzuri uliosaidia kuboresha Muswada huu. Hii inaonyesha ni jinsi gani sasa Watanzania kupitia Waheshimiwa Wabunge mmeona kuna umuhimu sana wa kukipa chombo hiki meno zaidi kwa sababu dunia inabadilika, uchumi unabadilika na ICT ni kitu dynamic wala siyo static. Kwa maana hiyo, nawapongeza na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuongoza vyema suala zima hili la utawala bora na kuwa championi kabisa katika ufanisi wa kusimamia utendaji kazi Serikali vilevile katika suala zima la ukusanyaji wa mapato. Sisi Watanzania tunaendelea kumuombea na kumuinua zaidi mbele za Mungu kwa sababu kazi anayoifanya ni njema na ni takatifu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitishwa kwa Muswada huu kutasaidia sana kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kwa urahisi na kwa gharama nafuu. Aidha, sheria ya Serikali Mtandao itasaidia kuondoa urudufu wa mifumo; kulinda usalama wa taarifa za Serikali na watumiaji; kupumguza gharama za kujenga, kuhudumia na kuendesha mifumo na kuwezesha mifumo kubadilishana taarifa na hivyo kuongeza tija na ufanisi wa utendaji kazi Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa Serikali Mtandao nchini baadhi ya mambo ambayo yametekelezwa yanaendelea kuleta faida mbalimbali ikiwemo kurahisisha ulipaji wa malipo mbalimbali na kuongeza mapato zaidi katika ku-control kwa maana ya ule mfumo wetu wa GPG; uombaji wa vibali ikiwemo vile vya kusafiri nje ya nchi kwa maana ya e-Vibali na vilevile kuanzisha e-Commerce kwa maana ya BRELA, TIC, TRA na kadhalika. Vilevile katika kuomba ajira Serikalini kwa maana ya Ajira Portal, kuomba mikopo katika elimu ya juu, udahili wa wanafunzi wa vyuo vikuu, matibabu mtandao kwa maana ya Telemedicine, Ofisi Mtandao kwa maana ya e-Office na utunzaji wa nyaraka kwa njia za kielektroniki kwa maana ya e-Record. Mifumo hii yote inapatikana kwa kutumia computer pamoja na simu za mikononi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa kuzingatia changamoto za mawasiliano na uwezo wa wananchi wengi kuwa na vifaa vya kisasa, mifumo mingi imeandaliwa ili iweze kupatikana kwa kutumia simu zisizokuwa na mawasiliano ya internet na hivyo kuwafanya wananchi wengi hasa wale walio vijijini kuwa na uwezo wa kupata huduma hizo. Nimeona katika michango mbalimbali ambayo imezungumzia inakuwaje kwa wale ambao wako vijijini, hili nitalitolea ufafanuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa mara nyingine tena nikushukuru wewe binafsi pamoja na Wabunge wote waliotoa maoni yao kwa njia ya maandishi na wale waliochangia kwa kuzungumza kama nilivyosema. Tunatambua michango na maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali mliochangia, tuna Mheshimiwa Saada, Mheshimiwa Mch. Msigwa, mama yangu Mheshimiwa Mwanne Nchemba, Mheshimiwa Bobali, Mheshimiwa Lulida, Mheshimiwa Mwakibete mdogo wangu, Mheshimiwa Lubeleje, Mheshimiwa Aida Khenani na Mheshimiwa Pascal Haonga na wengineo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ufafanuzi kwa ufupi wa hoja mbalimbali ambazo zimetolewa kama ifuatavyo na nitazungumza kwa ufupi sana. Kuna hoja ilioyokuwa imetolewa na Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu mwananchi wa kawaida atanufaika vipi na Sheria ya Serikali Mtandao. Serikali tumejipanga kwamba kila mwananchi sasa atapata huduma za Serikali kwa urahisi na kwa gharama nafuu popote pale alipo bila kulazimika kutembelea taasisi yoyote ya Serikali kwa kutumia simu yake tu ya mkononi hata kama ni katochi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine limezungumzwa tena na Kambi Rasmi ya Upinzani juu ya elimu ya watumiaji hususan wananchi. Wote tunaelewa kwamba elimu kwa umma ni jambo endelevu na behavior change ni process na sisi kama Serikali Mtandao hili jambo tumekuwa tukilifanya wakati wote na tutaendelea kulifanya kimkakati zaidi kwenye maeneo yote iwe ni kwenye social media, print media, TV na sehemu zote hata kama ni radio. Pia tumekuwa tukifanya mikutano na wadau mbalimbali katika kubadilishana mawazo kila mwaka. Kwa hiyo, haya yote tutaendelea kuyafanya kwa sababu ni endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine lilikuwa ni uanzishwaji wa community center na kiosk center vijijini kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi ambalo limezungumzwa na Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani. Serikali inatambua uhitaji wa center zote zilizotajwa na sheria hii inatoa fursa kwa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kuweka utaratibu wa uanzishwaji wa vituo hivi kwa kushirikiana na Waziri mwenye dhamana ya mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine lililozungumzwa na Mheshimiwa Saada ilikuwa ni mahusiano kati ya e-GA ya huku Bara na kule Zanzibar. Kwa kweli eGA imekuwa na ushirikiano wa karibu sana na Kurugenzi ya Serikali Mtandao Zanzibar na ushirikiano huu unaendelea kuimarishwa kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo limezungumzwa na Mheshimiwa Peter Msigwa ambapo amesema kwamba Muswada huu ni premature. Mimi nilikuwa naomba nimwambie mtumishi wa Mungu mwenzangu kwamba kwanza hili jambo ilipaswa tupongezwe kama Serikali kwa uthubutu na kama alivyosema Mheshimiwa Bobali tumechelewa kwa maana hili ni jambo zuri na kwenye uthubutu lazima kuwe na mwanzo na tumeweza ku-control mianya yote ya rushwa na ufisadi na ufanisi wa kazi katika kuboresha huduma kwa wananchi na wafanyabiashara maana siyo wananchi peke yake ni pamoja na wafanyabiashara ndio maana tuna e- Commerce.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile hili jambo ni 24/7 kwa sababu hata kama unataka kununua luku kama kuna jambo lolote sisi wote hapa ni mashahidi, hata kama umeme umekatika usiku unaweza ukanunua luku kupitia huu e-Mtandao. Vilevile unachukua ile *152*00# huduma zote unaletewa pale hata kama ungekuwa kijijini. Pia kunakuwa hakuna interaction kwamba lazima umuone mtu eti ndiyo uweze kupata huduma, kwa hiyo, hata kama ni usiku wa manane unapata huduma yako vizuri. Mifumo hii inaongea, haki inaongea, kwa maana hiyo huitaji kumuona mtu na ndiyo maana tunasema masuala ya rushwa hapa hakuna, ni ufanisi wa kazi kwa kusonga mbele na kanyaga twende Serikali ya Awamu ya Tano tumejipanga kuboresha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ilikuwa ni umuhimu wa usalama. Naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba tumepokea ushauri na tutauzingatia lakini Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi inaandaliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni yale matumizi ya mfumo wa open source na kama tunavyoelewa open source ni mfumo ambao unazingatia sana usalama wa taarifa za Serikali na hili tumekuwa tukilifanya. Ndiyo maana tunasema pamoja na taarifa za usalama Serikalini vilevile hata gharama zake zinakuwa ni ndogo na kupata mapato kwa kiwango cha juu zaidi kuko palepale na tunategemea tutaendelea kupata mapato zaidi kupitia Serikali Mtandao na data zetu zote za Kiserikali tutaweza kuzi-control.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Kambi Rasmi ya Upinzani na Wabunge wote kwa michango na maoni na ushauri uliowezesha kuboresha Muswada huu. Kama nilivyotoa ufafanuzi tutazingatia maoni yenu yote ambayo mmeyatoa na ushauri wote uliotolewa hususan kwenye utekelezaji wa sheria hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima, naomba kuwasilisha, ahsante. (Makofi)