Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Mwita Mwikwabe Waitara (5 total)

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nampongeza kiongozi wa Upinzani Bungeni Mheshimiwa Freeman Mbowe kwa swali zuri ambalo wewe mwenyewe Naibu Spika, umesaidia kuiua CCM humu ndani. Watu wataamini hizo hela mmekula, bora ungeacha ajibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nimwulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nitatumia maneno ambayo watawala wanapenda kuyasikia kwamba Serikali hii haijafilisika kabisa na Serikali hii ina mikakati mizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika Ubunge wangu wa muda mfupi huu, ile Sheria ya Mfuko wa Jimbo ndiyo sheria ambayo nimeona imekaa vizuri kweli kweli kwa sababu ni fedha ambazo Mbunge anapewa kwa taarifa tu zinaingia kwenye Halmashauri halafu Kamati yake inakaa, miradi inaibuliwa halafu wanapanga inaenda kwa wananchi moja kwa moja, Mbunge hagusi hata shilingi mia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali haijafilisika, tangu bajeti ya Serikali yenu hii ya Awamu ya Tano imepitishwa, Waheshimiwa Wabunge hawajapewa fedha hii ya Mfuko wa Jimbo. Sasa naomba unieleze, kama Serikali haijafilisika, Waheshimiwa Wabunge wameahidi miradi mbalimbali katika maeneo yao ya kiuongozi na wananchi wakawa wanasubiri miradi ile, Waheshimiwa Wabunge wanaonekana waongo kwa sababu fedha hazijaenda na Wabunge hawawezi kufanya maamuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini kauli yako juu ya hili? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimwambie kwamba Serikali hii haijafilisika. Mfuko wa Jimbo wa Mbunge ni miongoni mwa fedha zilizoandaliwa kwa bajeti ambayo tuliipitisha mwezi Julai, lakini Mfuko huu unapelekwa mara moja kwa mwaka kwenye Majimbo yetu. Nawe ni shahidi kwamba toka tumemaliza Bunge sasa tuna miezi mitatu. Bado tuna miezi kama saba ili kuweza kuhakikisha kwamba fedha yote tuliyokubaliana hapa inaenda kwenye maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo yana kipaumbele chake, yapo yale ambayo yanaweza kutekelezwa ndani ya mwaka mzima, lakini nataka nikukumbushe kwamba mfumo wa fedha zetu ni cash budget, tunakusanya halafu pia tunapeleka kwenye miradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe Mheshimiwa Mbunge faraja kwamba suala la Mfuko wa Jimbo bado unatambulika na fedha tutazipeleka kwenye Majimbo na Waheshimiwa Wabunge wote tutawajulisha tumepeleka kiasi gani ili sheria zile ziendelee kutumika na Mheshimiwa Mbunge kama Mwenyekiti wa Mfuko wa Jimbo utaendelea kuratibu mipango yako ya Jimbo lako na fedha ambayo tutaipeleka. Kwa hiyo, endelea kuwa mtulivu, fedha tutazipeleka na tutawajulisha Wabunge wote. Ahsante sana.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni sera ya Serikali kulinda raia na mali zao. Lakini mnamo tarehe 24 na tarehe 25, askari wa FFU katika Kambi ya Ukonga, Mombasa, walifunga barabara wakapiga akina mama, vijana na wazee na wakawatesa sana abiria na kuleta madhara makubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa ninaomba nipate tu, na wananchi wangu wasikilize, Serikali inatoa kauli gani juu ya matukio kama haya ambayo yanafanywa na viongozi na vijana ambao kimsingi tunatakiwa tuishi kama ndugu na kushirikiana kwa ajili ya kulinda raia na mali zetu? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Waitara, Mbunge wa Ukonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunazo taarifa kwamba pale Ukonga kulikuwa na mgongano mkubwa kati ya Jeshi letu la Polisi na raia, na mgongano huu umesababisha pia kuuawa kwa askari mmoja na watu wengi kupigwa, lakini hatua nzuri zimechukuliwa. Mkuu wetu wa Wilaya ya Ilala, Mheshimiwa Mjema, aliingilia kati na kuchukua hatua ya kuunda tume ambayo inafanya ufuatiliaji kuona chanzo na madhara yaliyojitokeza na wahusika katika jambo hili. Baada ya tume kumaliza kazi yake, ikibainika nani ametenda kosa hatua kali zitachukuliwa.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu wewe ni Mbunge wa eneo lile lazima utashirikishwa pia katika kupata taarifa za matokeo ya tume iliyoundwa na Mkuu wetu wa Wilaya ya Ilala, Mama Sophia Mjema.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naomba niseme kwa niaba ya wananchi wa Tarime Vijijini kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu ni Waziri Mkuu wa viwango; hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nataka nikwambie kwamba hotuba uliyotoa hapa Waheshimiwa Mawaziri na viongozi wakiifanyia kazi Wabunge hawa watafurahi sana na wananchi wetu watafurahi, ume-cover karibu kila eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu; pamoja na hotuba nzuri uliyotoa hapa, ninataka uwasaidie wananchi wa Tarime Vijijini, Serengeti, Bunda; ni lini hawa Mawaziri watakwenda kuwasikiliza wananchi wale ili kutoa elimu na kutambua ile GN ya mwaka 1968 ambayo kimsingi ndiyo kilio cha watu wangu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru Mheshimiwa Mbunge kutambua jitihada za Serikali katika kufanya utatuzi wa migogoro iliyopo kwenye Wilaya yake, Jimbo lake kule Traime Vijijini, Mkoani Mara, kwamba hatua iliyofikiwa sasa kwenye eneo lile ni kukutana kwa Mawaziri na wananchi ili kuwaelimisha, hayo ndiyo mahitaji makubwa ya wananchi wale, ili waweze kutambua kikamilifu mipaka iko wapi na wananchi wapate nafasi pia ya kuweza kuwasilisha hoja zao, mahitaji yao ili Serikali ifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa nilishawaagiza waende haraka, na ilikuwa ndani ya mwezi huu, lakini kutokana na majukumu tuliyonayo ndani ya Serikali na Mawaziri hawa kuwajibika kikamilifu, nataka nikuahidi, kuanzia tarehe 02 Mei baada ya sherehe za Mei Mosi ambazo wao pia watashiriki kule Morogoro, wataanza safari kwenda Tarime. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nina uhakika kwamba kati ya tarehe 03 na 04 watakuwa Tarime. Na tukualike wewe, tuwaalike Wabunge wa Bunda wanaoguswa na eneo lile la mipaka pamoja na Serengeti kushiriki vikao hivyo kwa sababu hoja zitakazotolewa na Mawaziri zitakuwa zinagusa kwenye maeneo hayo, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba risala ya Serikali kuhakikisha kwamba inatatua migogoro kati ya wananchi na maeneo yenye hifadhi za Serikali. sasa ningependa kujua nini mkakati wa Serikali kukomesha migogoro hii katika maeneo haya niliyoyataja?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Waitara Mbunge wa Tarime, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waitara analizungumza hili akijua kwamba tumelifanyia kazi sana pia kwenye eneo lake ambako kuna mgogoro wa wananchi na hifadhi; na tulliunda timu ya mawaziri walienda kwenye eneo lake. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie, kwamba mkakati wa Serikali wa kukomesha haya ni kushirikisha wananchi kwenye maeneo haya yote ambayo yamejitokeza na migogoro hii ili kuwa na mapitio ya pamoja ya mipaka ilipo kila mmoja ajue mpaka upo wapi. Serikali tumeagiza mamlaka hizi za hifahdi kuweka vigingi kama alama inayoonesha pande zote mbili kwamba hapa ndio ukomo wa watu kuingia kwenye upande mwingine; na vigingi hivi navyo tumesema viwe virefu siyo vile vidogodogo kirefu wapake rangi nyeupe kionekane kwa mbali ili kila mmoja apate kuelewa. Sasa jukumu hili tunapolifanya kwa kushirikiana pamoja tunaamini migogoro itapungua kwa sababu kila mmoja atakuwa anajua.

Mheshimiwa Spika, siku tatu/nne zilizopita hili limejitokeza sana kule Tarime ambako kata kadhaa na vijiji kadhaa kulikuwa na mgongano wa kutoeleweka kwa mipaka yake, na hili pia tumeona hata juzi siku mbili zilizopita kwa kutoelewana viongozi wa Serikali za vijiji walijiuzulu. Nafurahi kusikia pia jana viongozi wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Tarime wameenda kuwatembelea wananchi wamewaelimisha. Nawashukuru sana viongozi wale kwamba wamerudi kwenye nafasi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie wananchi wale ambao wako kwenye migogoro si Tarime lakini maeneo mengine yote, Serikali tunajipanga kufanya mapitio ya maeneo yote ili kuhakikisha kwamba hii migogoro haijirudii, lakini kila mmoja anakuwa na uelewa kwa kushirikisha na viongozi wale ambao wamerudi moja kati ya taarifa ambazo tumezipata ni kwamba wanahitaji kupata taarifa zaidi. Kwa ile Timu ya Mawaziri iliyoenda inakamilisha taarifa yake wataileta kwangu, tutaipitia kwa pamoja, tutashirikisha kwanza ndani ya Serikali, tutakwenda sasa Mkoa Mara, Wilayani Tarime mpaka kwenye vile vijiji. Tutakuwa na mikutano kwenye vile vijiji vya kuendelea kuelimisha zaidi kwa ukaribu na kuwashirikisha ili kila mmoja awe anajua. Sisi ndani ya Serikali tunaamini kwamba vijiji vyote, wananchi wote wanaoishi pembezoni mwa mipaka hii ya hifadhi watakuwa walinzi nambari moja wa kulinda hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutawajibika kwenda kutoa elimu maeneo yote. Tunajua hata hapa Kondoa kuna Pori la Mkungunero lina mgogoro, Babati, eneo la Tarangire lina mgogoro. Tunaambiwa Bunda pale katikati, katika ya Daraja na Mji wa Bunda pale kuna eneo lina mgororo, Serengeti nako pia kuna mgogoro. Haya maeneo yote tutayapitia eneo moja baada ya moja, tutakutana na wananchi, tutawaelemisha. Tunataka Watanzania tuone umuhimu wa hifadhi, lakini na sisi wahifadhi tuone umuhimu wa raia wanaokaa pembezoni mwa hifadhi. Tukiwa na dhana hii itatusaidia sasa kutunza rasilimali zetu popote zilipo kwa pamoja zaidi, wananchi pamoja na miundombinu tuliyonayo ndani ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa swali hili na huo ndio ufafanuzi wangu. Ahsante. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imetimiza sera muhimu ya uwekezaji nchini na hasa katika sekta ya madini. Katika kutimiza azima hiyo, wawekeza wamekuwa wakichukua maeneo ya watu maeneo kama kule Kabanga, Sumbawanga na kule Nyamongo, lakini maeneo hayo imechukua muda mwingi sana ama kuchelewa kulipwa au kutokulipwa kabisa fidia za wananchi.

Mheshimiwa Spika, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wananchi ambao maeneo yao yametwaliwa kwa muda mrefu na wawekezaji waweze kulipwa fidia yao na waweze kutimiza kupata haki yao ya kukaa katika maeneo hayo?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Waitara, Mbunge wa Tarime Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sera yetu, sheria za ardhi pamoja na uwekezaji nchini ziko wazi. Kwamba pale inapotokea mwekezaji yeyote anahitaji kutumia ardhi, ardhi ambayo ina mmiliki halali na shughuliki yake anaifanya, labda kwa kilimo, alijenga nyumba za makazi au uwekezaji kama ulivyosema, pindi ardhi hii inapotakiwa; iwe na Serikali au mwekezaji ni lazima apate fidia.

Mheshimiwa Spika, utaratibu unaotumika, baada ya kuwa mwekezaji ameomba kulitumia eneo hilo, uthamini utafanywa na mthamini wa Serikali, gharama zitapatikana na mhusika wa ile ardhi atahusishwa. Thamani ile ikishapatikana, kama ni Serikali, Serikali italipa, na kama ni mwekezaji atapewa ile gharama ya ule uthamini uliofanywa na atapaswa kulipa.

Mheshimiwa Spika, umetamka maeneo mengi, na mimi nimepata nafasi ya kupita maeneo kadhaa, tumekuta baadhi ya Watanzania waliokuwa wanamiliki ardhi kihalali wametoa ardhi yao kwa shughuli hizo za uwekezaji. Iwe ni kwenye madini au kwa shughuli nyingine yoyote ile ili mradi ni uwekezaji hawa wote wanapaswa kulipwa. Na nitoe wito kwa Wizara ya Ardhi ambayo ndiyo inasimamia sheria, kuhakikisha kwamba Watanzania ambao wanachukuliwa ardhi yao waliyomilikishwa kihalali, ni lazima walipwe fidia ya ardhi yao ili haki iweze kutendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ni muhimu sasa pia hata kwa mamlaka za Serikali za Mitaa pale ambako wananchi wapo wamechukuliwa ardhi yao kwa uwekezaji, kwa shughuli nyingine yoyote ile na wanahitaji kulipwa fidia, ni lazima haki yao waipate kwa kulipwa fedha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba inapotekea kuna madai kama bado madai yatolewe. Na hasa kama kumefanyiwa uthamini basi ile thamani ya ile ardhi au thamani ya ile mali iliyochukuliwa kwa ajili ya kupisha kwa shughuli nyingine ni lazima iweze kulipwa. Ahsante sana.