Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Jasmine Tiisekwa Bunga (1 total)

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali lifuatalo:-

Kwa kuwa Dira ya Maendeleo ya Nchi yetu ya Mwaka 2015 ni kufikia uchumi wa kati na uchumi wa viwanda ni kigezo kimojawapo; na kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imejielekeza kwenye uchumi wa viwanda na imejitahidi kutengeneza mazingira mazuri kwa wawekezaji ili waweze kuja kuwekeza; hata hivyo, wawekezaji wengi wanakwamishwa na kusumbuliwa sana:-

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu suala hili? Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jasmine kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli nchi yetu imejikita katika kuboresha uchumi wake kupitia viwanda ambapo tumetoa fursa kwa Watanzania kwa mtu yeyote kutoka Taifa lolote kuja kuwekeza hapa nchini. Suala la uwekezaji tumelipa nafasi muhimu sana kwenye uwekezaji hasa kwenye viwanda.

Awali tulikuwa tunatumia tu Taasisi ya Uwekezaji nchini, lakini Serikali imefanya maboresho makubwa kwenye uwekezaji pale ambapo Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli alipoianzisha Wizara Maalum ya Uwekezaji na kumteua Mheshimiwa Angellah Kairuki kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), kumteua pia Katibu Mkuu ili kusimamia uwekezaji kwa ukaribu zaidi.

Mheshimiwa Spika, lengo hapa ni kuhakikisha kwamba tunaondoa usumbufu ambao wanaupata wawekezaji hao ili kuweza kuwekeza kwa urahisi zaidi. Hata hivyo, kwenye uwekezaji sasa tumefikia hatua nzuri sana. Kwanza tumetengeneza andiko maalum (blueprint) ambayo imeonyesha njia rahisi za uwekezaji hapa nchini kwa lengo la kuondoa usumbufu kwa wawekezaji wetu. Kwa hiyo tumetengeneza mazingira rahisi ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, pili, tumeboresha kituo cha uwekezaji kwa kukaribisha Wizara zote zinazoguswa na uwekezaji kwa kuwa na mtu wao pale kwenye Taasisi ili mwekezaji anapokuja, huduma zote kama mtu alitakiwa kwenda Wizara ya Ardhi, mtu wa ardhi yuko pale; akitaka kwenda BRELA, mtu wa BRELA yuko pale; anakwenda sijui TFDA; mtu wa TFDA yuko pale. Kwa hiyo, tuna idara kama 10 au 11 ambazo ziko pale za kumhudumia mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, badaa ya kuwa Wizara ile imeletwa Ofisi ya Waziri Mkuu, tumeanzisha mfumo wa kielektroniki ambao mwekezaji sasa anaweza kuomba leseni kutoka popote alipo. Tunatambua kuna wawekezaji wako nje ya nchi, haimlazimishi yeye kuja moja kwa moja Tanzania kuanza kujaza makaratasi. Anajaza huko huko Marekani kuomba nafasi, kupata ardhi, kupata ithibati ya uwekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumetengeneza hayo yote kurahisisha mfumo wa uwekezaji kwa lengo la kupanua wigo wa uchumi hapa nchini kupitia viwanda, kilimo, madini na kila eneo ambalo mwekezaji anataka kuwekeza, sasa Tanzania imefungua nafasi, imetengeneza mazingira rahisi ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, natoa wito kwa Watanzania, kwa yeyote kutoka Taifa lolote kuja kuwekeza nchini Tanzania, fursa tunazo na ardhi tunayo. Fursa hizi sasa tumezikaribisha hata kwenye Mikoa na Wilaya kutenga ardhi kwa ajili ya kukaribisha wawekezaji ili pia kuendelea kuongeza mapato ya Halmashauri yenyewe, Mkoa wenyewe na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.