Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Catherine Valentine Magige (17 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa naomba niwashukuru akinamama wa Mkoa wa Arusha kwa kuniamini na kunipa kura kwa ajili ya kuwawakilisha Bungeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba nzuri aliyoileta wakati wa ufunguzi wa Bunge la Kumi na Moja. Hotuba hiyo iligusa maeneo mengi katika nchi yetu. Vilevile ilitupa mwelekeo na
dira ya Serikali ya Awama ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu, nimefarijika sana Mheshimiwa Rais aliposema kuwa Tanzania itakuwa nchi ya viwanda. Katika Mkoa wangu wa Arusha, miaka ya 1970 na 1980 kulikuwa na viwanda vingi sana vya Serikali
pamoja na watu binafsi kama vile Kiwanda cha Tanelec, Kiwanda cha Biskuti na cha Matairi cha General Tyre. Viwanda hivi vyote kwa sasa hivi havifanyi kazi, hali iliyopelekea madhara makubwa sana kwa wakazi wa Arusha na maeneo jirani na Mkoa wetu wa Arusha.
Mheshimwa Naibu Spika, Kiwanda cha Matairi cha General Tyre kilikuwa kiwanda kikubwa sana cha kuzalisha matairi Afrika Mashariki. Kiwanda hiki kilikuwa kimeajiri watu zaidi ya 400, kiwanda hiki kilikuwa kinaingiza mapato shilingi bilioni 100 kila mwaka na takwimu hizi ni kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2008. Kiwanda hiki kilifikia stage kikawa kinaajiri watu hadi milioni moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1971, Kiwanda cha General Tyre kilikuwa kiwanda namba moja Afrika Mashariki kwa kuzalisha matairi 1,200 kwa siku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kipindi hicho kiliweza kuzalisha matairi 1,200 kwa siku, sasa hivi tunashindwa kitu gani? Kwa sasa hivi soko la matairi lipo kubwa sana, kwa sababu tukianza kukitumia Kiwanda cha Matairi cha General Tyre, tutaanza na Serikali na taasisi zake zote kununua matairi ya General Tyre pamoja na mashirika ya Umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile soko la matairi bado kubwa sana, watu wengi sasa hivi wanatumia magari, magari yote hayo yanahitaji matairi. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ikianzishe upya Kiwanda cha General Tyre ili kiendelee kuleta mapato katika nchi yetu.
Kiwanda cha General Tyre kimepunguza ajira kwa vijana wa Arusha, wananchi wa Arusha, vijana wa Arusha, wanahitaji ajira, ajira hii itapatikanaje? Itapatikana kwa kurudisha viwanda vyetu ambavyo vilikuwa havipo tena. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Arusha hawaamini kama Serikali imeshindwa kufungua kiwanda kile. Wananchi wa Arusha tunaamini kuna hujuma za baadhi ya wafanyabiashara ambao wana-import matairi kutoka nje kwa ajili ya faida zao wenyewe hali ambayo inapelekea sisi kukosa uwezo wa kufungua kiwanda kile cha General Tyre.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa taarifa nyingi za kipolisi zinaonyesha ajali nyingi zinatokea kutokana na matairi yasiyokuwa na ubora ambayo tunayaagiza kutoka nje.
Tumekuwa tunapoteza ndugu zetu katika ajali kwa sababu ya matairi. Sasa naona ni wakati muafaka kwa Serikali kukifungua upya Kiwanda cha Matairi cha Arusha (General Tyre) ili tuweze kutumia matairi yale ambayo yana ubora. (Makofi)
Naomba niende moja kwa moja katika suala la maji. Tatizo la maji limekuwa kubwa sana kabla ya uhuru na baada ya uhuru. Kina mama wa Mkoa wa Arusha wamechoka kuhangaika na tatizo la maji. Kuna maji Ngorongoro, Monduli na Longido. Wamenituma niombe
Serikali yao, wanamwamini Mheshimiwa Magufuli, wanaimani kubwa na Serikali ya Mapinduzi.
Tunaomba sana kina mama hawa wa Arusha wasahau shida hii ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi wa maji wa West Kilimanjaro. Serikali ikitusaidia kuanzisha mradi ule vijiji kadhaa vitapata maji. Mradi ule tunaomba upelekwe mpaka Longido ambapo vijijini vya njiani kama Tingatinga, Singa, Kerenyai, Engiraret, Orbebe, Orpesi, Ranchi
mpaka Longido navyo vipate maji. Vilevile Monduli, Monduli kulikuwa na mabwawa matatu na yenyewe yamepasuka. Wananchi wa Monduli wanakunywa maji ya mabwawani pamoja na mifugo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana Serikali iangalie suala hili la tatizo la maji katika Mkoa wa Arusha. Naomba sana Waziri wa Maji unisaidie sana kutatua tatizo hili. Nakuamini najua ndiyo maana Mheshimiwa Rais wetu tunayemuamini akakuchagua, tunaomba utusaidie.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji. Kila siku wananchi wamekuwa wakiuwawa, mifugo imekuwa ikiuwawa lakini migogoro hii imekuwa haishi, nenda rudi migogoro hii inaendelea na wananchi wanazidi kuisha kwa ajili ya kufa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini sana wateuzi wa Rais, namwamini sana Mheshimiwa Lukuvi. Mheshimiwa Lukuvi nakuomba baada ya Bunge hili uje Mkoa wa Arusha kuna matatizo mengi ya ardhi, kuna tatizo la ardhi Loliondo, wananchi wamekuwa wakipata shida
hawajielewi, hatujui Serikali inataka nini, hatujui wanavijiji wanataka nini, hatujui wafugaji wanataka nini? Tunaomba sana Serikali iliangalie suala hili. Wananchi wamekuwa wanachomewa nyumba zao, mifugo yao inauliwa lakini sasa hivi Awamu ya Tano, tuna imani kubwa sana na Serikali na ukizingatia hotuba ya Rais wetu imeeleza kila kitu, tunaimani hawatatuangusha watatusaidia sana. (Makofi)
Naomba niongelee pia suala zima la Polisi. Polisi tumekuwa tukiwalaumu sana lakini vilevile Polisi wanaishi katika mazingira magumu sana. Nikitolea mfano Arusha Mjini kuna zile nyumba za Fire, ukipita pale ni aibu. Nyumba za Polisi ni chafu sana, ni nyumba ndogo na mnajua familia zetu za Kiafrika tunavyoishi. Polisi wale wanaishi katika mazingira ya shida sana na hata kwa kupita tu kwa mbali nyumba ni chafu sana. Tunaomba sana Serikali iangalie jinsi gani ya kuwasaidia Polisi katika suala zima la nyumba.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mabadiliko ya tabia nchi limekuwa linasababisha matatizo makubwa sana ya malisho ya mifugo pamoja na maji. Nakumbuka mwaka 2007 kulikuwa na ukame. Wilaya za Monduli, Longido, Ngorongoro, wafugaji walikosa malisho, mifugo
yao ilikuwa inakufa na wenyewe wakawa wanaishi kwa kuhamahama. Tunajua wafugaji wanaishi kwa kuhamahama siyo kwa kupenda bali kutokana na mazingira wanayokuwepo, unakuta mifugo yao haipati maji, haipati huduma kwa hiyo, inabidi wahame. Mheshimiwa
Waziri wa Ardhi, tunaomba sana mliangalie wafugaji wa Mkoa wa Arusha kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana hotuba ya Rais imegusa mambo mengi sana. Nashangaa sana watu wanapokaa na kuikejeli hotuba ya Rais. Mmeona hata juzi Mheshimiwa Magufuli amefika Arusha wananchi walivyomlaki kwa furaha. Mbunge mwenzangu wa Arusha pale awe makini sana, kwa kauli alizozitoa hapa wananchi wa Arusha wanaweza wakampiga mawe na kumzomea kwa sababu wamemkubali Magufuli na Serikali ya Chama cha CCM.
Nilitegemea Mbunge mwenzangu atasimama na kumsifu Mheshimiwa Rais Magufuli na kusifu wananchi wa Tanzania pamoja na wananchi wa Mkoa wa Arusha kwa kumpa kura za kutosha Rais Magufuli. Naomba sana tukubali, upinzani siyo kupinga kila kitu. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu. Kwanza kabisa, naomba nielekeze mchango wangu kushukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuanza kutimiza ahadi zake ambazo aliahidi kipindi cha kampeni. Aliahidi shilingi milioni 50 kila kijiji, tumeona zimeanza kwenda, tunashukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Shilingi milioni 50 hizi za kila kijiji tumeona wanawapa Baraza la Wawekezaji, ni mpango mzuri sana. Hata hivyo, tunaomba Baraza la Wawekezaji wahakikishe wamepita kata hadi kata ili fedha hizi zifike kwa walengwa.
T A A R I F A....
Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa yake kwanza naikataa.
Fuatilia vizuri, naona Magufuli anawapa moto na hiyo ni bado. Arusha tumeshachukua kata, tumeshaanza kuchukua mitaa…
Tulieni, tulieni. Mheshimiwa Naibu Spika, ulinde muda wangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana jembe Rais Magufuli, Rais wa wanyonge, Rais wa maskini, sasa hivi maskini wote wanaimba Chama cha Mapinduzi kwa sababu ya Rais Magufuli. Hongera sana Rais wetu na Arusha tutarudisha Majimbo kwa hii kasi ya Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kutoa mchango wangu, tunaomba sana hizi shilingi milioni 50 za kila kijiji, Wabunge wa maeneo husika hasa wa Chama cha Mapinduzi tushirikishwe ili tujue zinapoenda na vilevile sisi ndiyo ambao tunajua watu ambao wanahitaji fedha hizi. Tunaomba zile asilimia tano ambazo zilikuwa kwenye Halmashauri kwa ajili ya akinamama na vijana ziendelee kuwepo, siyo shilingi milioni 50 itoke zile zisiwepo, ziendelee kuwepo kama sheria inavyosema.
Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze katika suala zima la elimu. Tumeona Serikali ya Chama cha Mapinduzi imesema elimu bure. Mpango huu umesaidia sana watoto wa maskini sasa hivi wanapata elimu. Watoto wengi wa maskini walikuwa wanachukuliwa wakiwa wadogo kwenda kufanya kazi za ndani, lakini sasa hivi tunaona Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeleta usawa kwa watoto wetu na imeleta usawa kwa maskini na matajiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili ni zuri sana ingawa lina changamoto chache. Tumeona baadhi ya shule za kutwa wazazi wanaendelea kutoa fedha kwa ajili ya chakula. Tunaomba sana Serikali yetu sikivu chini ya Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli irekebishe suala hili ili watoto waweze kupata mlo shuleni wazazi wasiendelee kutoa michango.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nije katika suala zima la madawati. Naipongeza sana TAMISEMI kwa jinsi inavyoshughulikia suala la madawati. Katika Mkoa wangu wa Arusha kulikuwa na tatizo la madawati 24,304 lakini uongozi wa Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya za Mkoa wa Arusha wamejitahidi mpaka sasa hivi wameshakusanya madawati zaidi ya 18,000. Tatizo la madawati lililobaki kwa sasa hivi kwa shule za msingi ni kama madawati 6,000. Naomba sana tuendelee kusaidiana katika suala hili hata kwa mikoa mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende katika suala zima la afya. Naomba Serikali ilitoe suala la afya TAMISEMI ili Wizara hii ijitegemee waweze kughulikia matatizo ya wananchi kiundani zaidi. Naomba niendelee kwa kumpongeza Mkuu wangu wa Mkoa wa Arusha kwa jitihada ambazo amekuwa akizionesha katika suala zima la afya. Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wameweza kukarabati Kituo cha Afya cha Ngarenaro, Hospitali yetu kubwa ya Mount Meru wamefungua duka la dawa pale la MSD na limeshaanza kufanya kazi, Hospitali ya Kaloleni wameikarabati na sasa hivi ninavyoongea wanaendelea na Hospitali ya Levorosi, nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba Serikali iuangalie sana Mkoa wangu wa Arusha, Wilaya ya Ngorongoro hasa Hospitali ya Loliondo inayoitwa Waso. Hospitali ile imekuwa ikipokea wagonjwa wengi sana na akinamama wajawazito, lakini kwa sababu eneo lile ni la wafugaji akinamama wamekuwa wakiacha wagonjwa wao kwenda kuwatafutia chakula nyumbani wakati mwingine wanakwenda umbali wa kilometa mpaka tatu. Naiomba Serikali katika bajeti yake ya Hospitali ya Loliondo ya Waso watuwekee chakula ili wagonjwa wawe wanapata chakula pale pale na wawe na matumaini makubwa na Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hili suala la ugonjwa wa endometriosis ambapo tumemwona mwanamitindo maarufu kama Millen Magese amejitokeza hadharani na kukubali kuwa anaumwa endometriosis. Ugonjwa huu ni mbaya sana kwa watoto wetu wa kike na wanawake kwa ujumla kwani unapelekea utasa. Mwanamitindo huyo amejitokeza na anapita mpaka kwenye shule kuelezea kuhusu ugonjwa huu, ni ugonjwa ambao unaweza ukamkuta ndugu yako, dada yako au watoto wetu. Tunaomba sana Serikali ielezee kiundani kuhusiana na ugonjwa huu, athari zake na vilevile watoto wetu wa kike wapate matibabu ya ugonjwa huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla na Makamu wetu wa Rais, mwanamama Mheshimiwa Samia, tumeona wamemuunga mkono mwanamitindo huyu kwa ajili ya kuelimisha jamii nzima ya Watanzania hususani watoto wa kike ili waelewe tatizo hili na jinsi ya kujikinga maana wakijikubali kama mwanamitindo huyo nadhani watakuwa free kueleza tatizo lao na kutibu ugonjwa huu ambao unapelekea utasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Ilani yetu ya Uchaguzi tuliahidi bima ya afya kwa kila mwananchi. Tunaomba sana Serikali ilete Muswada huu Bungeni mapema ili tuweze kuupitisha, wananchi wetu waweze kupata huduma ya afya kupitia Serikali yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana Serikali iangalie upya suala zima la ugonjwa wa kisukari. Ugonjwa wa kisukari hasa huu wa kurithi, tumeona watoto wadogo wanapata sukari na zimekuwa zikiwatesa sana. Wananchi waelimishwe watajikinga vipi na kisukari, tumeona hata watu wazima, wanaume wanaachwa mpaka na wake zao kwa sababu ya ugonjwa huu wa sukari.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali i-take serious ugonjwa huu, kwa kweli wananchi wanapata shida, akinamama wanapata shida kwa sababu wanaume zao wanakuwa na ugonjwa wa sukari. Tunaomba sana Serikali iangalie kwa makini ugonjwa huu na kuelimisha watu jinsi ya kujikinga na itawasaidia vipi kaka zetu na baba zetu katika suala zima la ugonjwa huu wa kisukari.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba safari hii fedha za miradi ya maendeleo ziende kama ilivyokusudiwa. Tumeona katika sekta ya afya hususani kwenye vituo vya afya na maeneo mengi fedha za maendeleo hazifiki kama zilivyokusudiwa na hivyo kuzorotesha shughuli za maendeleo. Tunaomba sana Serikali ifikishe fedha za maendeleo kama ilivyopangwa kwa sababu tumekuwa tunapata matatizo mengi lakini fedha haziendi kama ambavyo zimekusudiwa. Tunaomba Serikali ihakikishe inafikisha fedha hizi kama ilivyopangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kumshukuru Rais wetu John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za kutumbua majipu, tunamuunga mkono aendelee na kazi hiyo ya kutumbua majipu. Tunaona wananchi wanamkubali, tumeanza kuirudisha Arusha kidogo kidogo, mitaa Arusha tumepata, yote hii ni kutokana na kwamba wananchi wanakubali utendaji wa Rais wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwenye macho haambiwi tazama, lakini ndiyo hivyo Serikali ya CCM iko juu na tukiendelea hivyo tutarudisha majimbo yetu yote na watu wa Arusha siku hizi hata nguo za kijani tunavaa na tunashangiliwa tunaambiwa Hapa Kazi Tu. Tunaomba waendelee kuboresha hospitali zetu ili Chama chetu cha Mapinduzi ambacho ni cha ukweli, kinatekeleza ahadi, kinawajali maskini na ambacho mafisadi walikikimbia wenyewe walivyoona moto wake kiendelee kukubaliwa na wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu katika uchumi wa nchi yetu. Naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Hifadhi la Taifa (TANAPA) ni miongoni mwa mashirika ya umma yanayotuingizia pesa nyingi sana katika nchi yetu. Utalii katika nchi yetu unachangia 18% ya GDP ya Taifa. Jambo la ajabu na la kusikitisha sana, miaka zaidi ya mitatu TANAPA haina Bodi ya Wakurugenzi. Maamuzi muhimu yamekuwa yakitolewa na viongozi wa Wizara akiwemo Waziri na Makatibu Wakuu walioondoka na hata wa sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, miaka kadhaa kulitokea mvutano juu ya ada zinazotakiwa kulipwa na wenye mahoteli maarufu kama concession fee, walishtakiana wakapelekana Mahakama Kuu na TANAPA walishinda kesi ile lakini mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea kwa sababu hakuna Bodi ambayo ndiyo ilitakiwa wapange jinsi gani ada hizi zitatozwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunapoteza mapato mengi sana kutokana na kukosa hizi fee za kwenye mahoteli. Kwa mwaka TANAPA inapoteza shilingi bilioni 10 kwa kukosa fees hizi. Shilingi bilioni 10 siyo pesa ndogo, ni pesa nyingi sana. Tunaona Rais wetu anavyohangaika kutafuta pesa, anabana matumizi, shilingi bilioni 10 hizi zingeweza kupeleka maji Arusha, Karatu, Longido, Ngorongoro na zingeweza kusaidia watoto wa maskini wakakaa kwenye madawati. Sijui ni kwa nini mpaka sasa hivi pesa hizi hazijaanza kukusanywa na ni kwa nini Bodi ya TANAPA mpaka sasa hivi haijaundwa. Waziri atakapokuja ku-wind up naomba aniambie ni lini Bodi ya TANAPA itaundwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA Ndugu Allan Kijazi kwa sababu amekuwa akimsaidia Rais kusaidia maskini. Tumeona juzi wamemkabidhi Mheshimiwa Makamu wa Rais shilingi bilioni moja kwa ajili ya madawati kwa mikoa 16, tunamshukuru sana kwa hilo. Nimeona nikitaja TANAPA bila kumtaja Ndugu Allan Kijazi nitakuwa sijaitendea haki hotuba yangu, nampongeza sana, naomba aendelee hivyo hivyo kum-support Rais wetu kuwa sasa ni kazi tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba moja kwa moja niende katika suala zima la ujangili. Ujangili umeshamiri sana, wanyamapori wamekuwa wakiuawa, tembo wapo hatarini kutoweka licha ya Serikali pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kufanya jitihada za kutatua tatizo hili. Majangili wana silaha kali sana hasa katika mapori yetu kama Ugala, Loliondo na mapori mengine mengi. Mbaya zaidi sheria haziruhusu walinzi wa makampuni ya vitalu vya uwindaji na YWMA kutumia silaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, naona sasa hivi ni wakati muafaka wa kuleta sheria ili walinzi wa haya makampuni waruhusiwe kutumia silaha kwenye hifadhi zetu ili washirikiane na walinzi wa wanyamapori na wa TANAPA, majangili wamekuwa wakitamba sana kwenye hifadhi zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba iwekwe adhabu kali sana kwa ajii ya majangili siyo kuwa watozwe fine tu hapana, majangili wana pesa nyingi, fine kwao ni kitu kidogo. Tumeona Serikali ya Kenya wameweka sheria atakayekutwa kwenye hifadhi bila kibali anapigwa risasi sisi hata kama hatuwezi kufanya hivyo, lakini ni wakati muafaka wa Serikali kuleta sheria hapa Bungeni ikiwezekana majangili wafungwe kifungo cha maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia inasemekana kuwa baadhi ya Wabunge ni majangili, wamekuwa wanajihusisha na biashara hii ya ujangili.
Nina imani hakuna ambaye yupo juu ya sheria. Hata gazeti la Jamhuri la leo limeandika Mbunge jangili. Huyo Mbunge jangili ni nani, ni Munde Tambwe, Catherine Magiga au Ally Keissy, tunataka tufahamu. Vyombo vya usalama, vyombo vya sheria vipo wafuatiliwe ijulikane Mbunge jangili ni nani. Hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria na akikutwa kiongozi ambaye ni jangili kama Mbunge jangili ,naomba mfano uanze kuoneshwa kwake. Siyo tunalaumu tu watu wengine wakati majangili tuko nao humu humu ndani, tunataka kuwafahamu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi majuzi gazeti ya Jamhuri liliandika makala ikaonesha jinsi vibanda vinavyokusanya mapato ya watalii kwenye mapori ya Loliondo na Longido, vibanda vile vilikuwa vinasikitisha sana, ni vibanda vya miti tu. Kweli watalii wanatuletea dola wanakuta watu wamekaa kwenye vile vibanda wanapokea mapato tuko serious na utalii wetu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua Wizara haihusiki zinazohusika ni Halmashauri ya Longido na ya Monduli lakini mtalii anapokuja hazitambui zile Halmashauri bali Wizara ya Maliasili, naomba tuwe serious kwa hili. Tunataka kupokea dola za watalii, tunapokea kwenye vibanda, vibanda vya ajabu, ni aibu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja naomba nielekeze mchango wangu katika misitu. Misitu inamalizwa, biashara za mkaa zimeshamiri sababu kubwa wakisema bei ya gesi au nishati mbadala ni kubwa. Naomba suala hili la mkaa ingawa kwa Wizara ni suala mtambuka lakini bado kuna ukweli misitu yetu ambayo iko chini ya Maliasili watu wanakata mikaa wanaimaliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali iliangalie sana suala hili la kukata misitu na iwachukulie hatua ambao wanauza mikaa, maana wanakata miti bila vibali na sasa hivi tumeona magari yanasafirisha mkaa usiku kwenye ma-container. Naweza nikatolea mfano pale kwa Msuguli kuna watu wanakaa pale kwa ajili ya kukagua hizi lumbesa za mazao sasa huoni kama ni wakati muafaka watu wa misitu nao wakawepo pale kwa ajili ya kuhakikisha kuwa miti yetu haikatwi ovyo na kukwepa kodi kupitia misitu? Tunaomba sana Serikali iangalie suala hili zima la mkaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona hapa watu wanaongelea kuhusu ndege, mimi akinamama wa Arusha hawaniulizi kuhusu ndege, wanauliza kuhusu maji na mitaji. Kwa hiyo, naomba tujielekeze sana kuona haya masuala ambayo ni muhimu kwa ajili ya wananchi wetu, siyo tunajiangalia sisi tu maana wale wapiga kura kule hata ndege hawapandi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba TANAPA iendelee kuwasaidia vijana na akinamama kwa kuwapa mitaji. Kuna akinamama na vijana wengi ambao wanafanya biashara ya utalii hasa katika Mkoa wangu wa Arusha iwasaidie kuwapa semina wapate elimu ya ujasiriamali ili waweze kutumia vizuri fursa hii ya utalii. Vilevile wawatafutie masoko, kuna akinamama wanauza shanga na vinyago kwa watalii watusaidie akinamama hao wapate soko ili waweze kujitosheleza na mahitaji yao mbalimbali kama ya kusomesha watoto wao na waweze kufanya biashara za kiutalii na wanufaike na utalii wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ila naomba tu Waziri atakaponijibu aniambie ni lini ataunda Bodi ya TANAPA, la sivyo nitatoa shilingi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) ni miongoni mwa mashirika ya umma yenye kulisaidia Taifa kupata fedha nyingi za kigeni. Utalii nchini mwetu unachangia asilimia 18 ya GDP na sasa kiasi hiki kinaweza kuongezeka zaidi. Jambo la ajabu, TANAPA kwa miaka zaidi ya mitatu sasa haina Bodi ya Wakurugenzi. Mambo yote yamekuwa yakiamriwa na viongozi wa Wizara yaani Waziri na Katibu Wakuu waliopita na waliopo sasa. Hii ni hatari kwa shirika kama hili lenye fedha nyingi zinazohitaji utaratibu wa Bodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujangili unashamiri, idadi ya wanyamapori ni kubwa mno. Tembo wako hatarini kutoweka licha ya juhudi za Serikali na vyombo vya ulinzi na usalama katika kukabiliana na hali hiyo. Majangili wana silaha hasa katika mapori kama ya Ugalla, Moyowosi, Loliondo na mengine mengi. Mbaya zaidi sheria haziruhusu walinzi wa kampuni zenye vitalu vya uwindaji katika mapori ya akiba na WMA kuwa na silaha. Hali hiyo imesababisha majangili watambe. Kwa nini Mheshimiwa Waziri asilete sheria Bungeni ili walinzi hao wapewe silaha na kwa hiyo, wasaidiane na wale wa TANAPA na wa wanyamapori kukabiliana na ujangili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, adhabu kwa majangili zisiwe faini, bali ziwe hukumu za kifungo cha maisha. Kenya wana sheria kali zinazosaidia sana kulinda wanyamapori wao. Kwa mfano, wao mtu akipatikana ndani ya hifadhi kinyume cha sheria, wanampiga risasi. Sisi tunaweza tusiwe na adhabu ya aina hiyo, lakini wakati umefika kwa Serikali kuleta hapa Bungeni mabadiliko ya sheria ili majangili wajue tumedhamiria kukomesha vitendo vyao. Serikali isiwe na kigugumizi cha kuwashughulikia viongozi wanaotajwa kuwa ni washiriki wakuu wa ujangili. Yapo maneno kuwa hata miongoni mwetu Waheshimiwa Wabunge kuna majangili. Kama kweli wapo, ni vizuri sheria zikatekelezwa badala ya kuendelea kuwaaminisha wananchi kwa maneno tu kuwa kuna Waheshimiwa Wabunge majangili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka kadhaa iliyopita kulitokea mvutano kuhusu ada wanazopaswa kulipa watu wenye hoteli (concessions fee). TANAPA walifungua kesi katika Mahakama Kuu na kushinda kesi hiyo. Ikaamuliwa wenye hoteli walipe, lakini utekelezaji wake ulipaswa uanze kwa Bodi kukaa na kupanga viwango vya ada hiyo. Sasa miaka zaidi ya mitano uamuzi huo haujatekelezwa na haujatekelezwa kwa sababu hakuna Bodi. Kwa kutoweka ada hizo, TANAPA wanapoteza wastani wa shilingi bilioni 10 kwa mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ahakikishe anamshawishi Mheshimiwa Rais mapema iwezekanavyo ili Bodi ya TANAPA iundwe; na kwa kufanya hivyo, iweke viwango vya ada na utekelezaji uanze mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mifugo katika mapori ya akiba, mapori tengefu, WMA na Hifadhi za Taifa ni mingi sana. Mapori kama Maswa, Moyowosi, Kijeleshi, Ugalla yanaelekea kufa. Pori tengefu la Loliondo limevamiwa na malaki ya mifugo kutoka nchi jarani (Kenya). Loliondo ni kama imekufa. Shughuli za kibinadamu zikiwamo za kilimo ni kubwa mno. Wanyamapori wamekimbia, Loliondo hii ni buffer zone ya Serengeti na eneo ambalo ni mazalia ya nyumbu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mifugo imekuwa mingi sana kiasi cha kufikia hatua sasa ya kuona hatari siyo ujangili tu, ila mifugo katika mapori ya hifadhi. Pamoja na umhimu wa mifugo katika nchi yetu, Serikali isisite kutekeleza Operesheni Ondoa Mifugo ambayo imepangwa kuanza tarehe 15 Juni, 2016. Bila kufanya hivyo rasilimali wanyamapori itatoweka katika nchi yetu na hii itakuwa aibu kubwa kwa kizazi kijacho na ulimwengu kwa jumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuweke kando siasa na tujikite kwenye uhifadhi. Faida za uhifadhi ni kubwa; kwa mfano, nyati mmoja anayewindwa anaiingizia Serikali zaidi ya shilingi milioni tatu. Simba mmoja anaingiza zaidi ya shilingi milioni 10. Kwa hiyo, tusiifanye mifugo ikawa mbadala wa wanyamapori kwa sababu faida yake ni kwa wachache wenye kuimiliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Gazeti la Jamhuri lilitoa makala ikionesha vibanda vibovu kabisa vya kukusanya mapato kutoka kwa watalii katika maeneo ya Oldonyo Lengai na Engaruka. Ile ni aibu kubwa kwa sababu vibanda vyenyewe vimeshikiliwa na nguzo za miti visianguke. Hata watalii watatushangaa kuona dola zinakusanywa kwao na watu walio kwenye vibanda vibovu. Ingawa vibanda hivyo vipo chini ya Halmashauri za Longido na Monduli, bado Wizara ya Maliasili na Utalii inapaswa kuitazama aibu hii na kuiondoa kwa sababu watalii hawazijui Halmashauri hizo, isipokuwa Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya mkaa inashamiri sana. Misitu inamalizwa na sababu inayotolewa ni kuwa bei ya gesi au nishati mbadala ni kubwa. Ingawa suala hili la mkaa ni mtambuka Kiwizara, bado ukweli unabaki kuwa mkaa mwingi unatolewa katika mapori yanayohifadhiwa kisheria chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Mbaya zaidi, hata huo mkaa unaouzwa watu wengi hawalipi ushuru. Malori ambayo kisheria hayaruhusiwi kusafirisha mkaa, leo yanasafirisha hadi kwenye makontena nyakati za usiku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pale Dar es Salaam watumishi wa Wizara wakae kwenye maegesho pale kwa Msuguri ili kuyakamata malori yote yanayopakia na kusafirisha mkaa bila vibali wala kulipa ushuru. Watumishi wa Wakala wa Vipimo wapo hapo sasa wakidhibiti upakiaji wa lumbesa kwa mazao kutoka mikoani. Sioni kwa nini Wakala wa Misitu nao wasikae hapo kwa Msuguri ili kuyadhibiti malori haya yanayotumika kutenda makosa haya ya uhifadhi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kazi kubwa inazofanya dhidi ya kukwamua kiuchumi wananchi wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea suala zima la afya hasa katika Mkoa wangu wa Arusha katika Wilaya ya Longido, wananchi walio mpakani mwa nchi jirani ya Kenya maeneo ya Namanga wamekuwa wakivuka mpaka na kwenda kutibiwa nchi jirani ya Kenya. Jambo hili limekuwa kero sana kwa wananchi wa Wilaya ya Longido. Tunaomba Serikali iwasaidie wananchi wa Longido kuwajengea hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Arumeru Magharibi ni jimbo kubwa sana hali inayopelekea wananchi wengi kutofikiwa na huduma muhimu. Naomba Serikali iangalie upya jinsi ya kugawa jimbo hili ili wananchi wengi waweze kufikiwa na huduma muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo hili kumekuwa na migogoro ya ardhi mara kwa mara na migogoro hii inapelekea wananchi kuishi bila amani. Kuna baadhi ya wawekezaji wamejilimbikizia ardhi kubwa na wanatumia tofauti na ilivyokusudiwa. Wananchi wana shida ya ardhi
huku wawekezaji wamejilimbikizia ardhi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo hili la Arumeru Magharibi kuna tatizo kubwa la akinamama ambao wamekuwa wakitembea mwendo mrefu kutafuta maji. Naiomba Serikali iangalie kwa ukaribu changamoto nyingi zilizomo katika jimbo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jimbo hili lina changamoto kubwa ya barabara, barabara zake ni mbovu. Naiomba Serikali iliangalie hili ilki wananchi wake wafaidike na Serikali yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza kabisa naomba nianze kwa kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayofanywa ya kuendeleza miundombinu ikiwemo ya barabara. Naomba nitoe shukrani zangu kwa kuwa tumeona Arusha inazidi kukua, tumeona barabara ya Tengeru mpaka Sakina kilometa 15, tumeona by-pass ndani ya Jiji la Arusha ambayo inaendelea kupunguza msongamano katika jiji la Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa kuliko yote naomba niishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa barabara ya Ngorongoro. Tumeona barabara ya lami ya kilometa 50 inayofika mpaka Waso ambayo ni kiwango cha lami. Barabara hii itawasaidia sana akina mama wa Arusha katika kufanya biashara zao hasa Ngorongoro kwa ajili kusafirisha bidhaa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende moja kwa moja katika masuala ya anga. Tumekuwa tukidhiakiwa na kupata aibu kuambiwa tunazidiwa na nchi ndogo kwa ajili ya ndege, lakini tumeona kazi aliyoifanya aliyofanya Mheshimiwa Rais kwa kutuletea ndege. Tumeona upande wa pili walikuwa wanasema shirika limekufa, likafufuliwa, tumeletewa ndege wakawa wanasema ndege hazijaja, sasa hivi ndege zimekuja wameingia wanansema kuna ufisadi katika manunuzi, jamani hivi hawa watu wanataka nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunamwambia Mheshimiwa Rais wetu afanye kazi kwa sababu kelele za chura hazimzuii ng’ombe kunywa maji. Vilevile tunajua kabisa mwanaume wa kisukuma amewashika pabaya, na bado, itakapofika mwaka 2020 wataendelea kulialia kwa Watanzania na ndipo Watanzania watakapoamua, kwamba watafuata machozi au watamrudisha mwanaume wa Kisukuma? Amewashika pabaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba moja kwa moja nielekeze mchango wangu katika Uwanja wa Ndege wa Arusha. Bajeti iliyopita walisema watakarabati Uwanja wa Ndege wa Arusha kwa kuongeza sehemu ya kugeuzia ndege na ya kurukia, lakini mpaka sasa hivi bado haujaongezwa; tumesahau kuwa Arusha ni Jiji la kitalii na watalii wengi wanatumia ndege zetu kwa ajili ya kuingia na kutokea Arusha. Kwa hiyo tumekuwa tukikosa mapato mengi kutokana na watalii wetu ambao wanaanzia Dar es Salaam au wanaanzia KIA, watalii ambao wanakwenda Kanda ya Kaskazini ikiwemo na Arusha.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri aniambie kwa sababu mwaka wa jana kulikuwa na uwanja wa Ndege wa Arusha lakini sasa hivi sijaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba moja kwa moja nijielekeze kwenye……

T A A R I F A . . .

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza taarifa yake siitaki, anaelewa kabisa mwanaume wa Kisukuma anayewasumbua ni Rais John Pombe Magufuli, sina haja ya kumwambia, anatafuta kiki, Magufuli anawasumbua sana na bado kwa kazi kubwa anayofanya ya kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi. Tunajua hamlali kwa ajili yake, mnamchafua halafu mnakuja kumuomba barabara, hebu tulieni huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye Shirika la Posta ambalo limekuwa likiwalipa waliokuwa wafanyakazi wa Jumuiya ya Posta ya Afrika Mashariki ambao wanalipwa kwa niaba ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaomba Serikali iwalipe zile pesa ambazo walikuwa wanawalipa Shirika la Posta, shilingi bilioni nne wawalipe ili na wenyewe waendelee kujiendesha vizuri.

Tumeona reli ya standard gauge inakuja, ambayo itatusaidi sana wamekuwa wakiikashifu lakini hiyo italeta maendeleo kwa wananchi na hatimaye wananchi wanatuuliza maendeleo. Tunajua, tunaposema mwanaume wa kisukuma linawauma sana kwa sababu mwanaume wa kisukuma ambaye ni kiongozi wetu Tanzania nzima ni mmoja na anafanyakazi na ni Rais wetu John Pombe Magufuli, anatekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, anaendelea kuleta maendeleo na Watanzania wote wanajua hata…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Mchango wangu nitauelekeza moja kwa moja katika Shirika letu la Ndege la ATCL. Katika vipindi viwili vya 2016/2017 na mwaka 2017/2018, tumeona imetengwa karibu shilingi trioni moja kwa ajili ya ATCL ambapo kwa kila kipindi itakuwa shilingi bilioni
500. Uwekezaji huu ni mkubwa mno na unahitaji umakini wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ili ATCL ipate faida, ni lazima twende sambamba na uwekezaji katika mambo makuu mawili. Jambo la kwanza ni uwekezaji wa ndege kama hivi tunavyofanya sasa hivi; jambo la pili ni kuwekeza katika uendeshaji wa ATCL, yaani mtaji wa kazi na rasilimali watu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa ndege, naomba nimpongeze sana Mhshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutuletea ndege za kisasa na ametuhakikishia ni salama kabisa. Itakapofika mwaka 2020 kama siyo 2019 zitakuwa ndege saba. Nampongeza sana Rais wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wasiwasi mkubwa unakuja kwenye uwekezaji katika uendeshaji wa ATCL. Tumezoea tukinunua tu ndege tunaacha, tunajua tayari tumeshanunua ndege bila kuwekeza. Tunategemea kupata faida, lakini hatuwezi kupata faida tu bila kuiwezesha ATCL iweze kuendesha biashara ya ndege. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunajua kuwa ATCL ilibaki jina tu, haikuwa inafanya vizuri, ndege zake zilikuwa hazieleweki, lakini sasa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kaanza kuturudishia ATCL mpya. Vilevile haikuwa na rasilimali watu na mtaji; naongelea kwa upande wa kujiendesha. Kwa hiyo, lazima tuisaidie ATCL kujiendesha ili iwe kibiashara zaidi. Tunajua ATCL ilikuwa ni jina tu au Kampuni isiyokuwa na rasilimali watu wala chochote; tunajua kwa sasa hivi ATCL kitu ambacho inahitaji ni working capital na siyo startup cost. Ni wazi kwamba bila kuiwezesha ATCL haitaweza kujiendesha yewenye na haitaweza kujiendesha kibiashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uwekezaji uliofanywa na Serikali ni mkubwa mno, lazima uambatane na uwekezaji wa kuiendesha ATCL ili iweze kutoa huduma nzuri. Tumeanza kuona mabadiliko ya ATCL, tumeona safari hazikatishwi, tumeona inaenda vizuri sana. Vilevile naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutuletea Mtendaji anayeweza hii nafasi, ana uzoefu. Ni muda mfupi sana naweza nikasema ametuonyesha wonders. Naomba sana tum-support Mtendaji huyu Ledislaus Matindi kwa kazi kubwa anayofanya, ana uzoefu na anajua changamoto za ATCL. Lazima tuunge juhudi za Serikali mkono na tuwe wazalendo kwa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Mheshimiwa Rais ameteua Bodi nzuri; lazima tuhakikishe Bodi na Menejimenti wamejikita zaidi kuisaidia ATCL ijiendeshwe kibiashara na siyo kukaa tu kusema kuwa ni Shirika la Serikali. Hatuna wasiwasi na matumizi ya fedha kwa sababu ya uongozi uliopo sasa hivi tunauamini, tunajua hata tukiwawezesha mapato yataenda vizuri, fedha zitatumika kama zilivyokusudiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tujifunze kwa wenzetu ambao waliweza kuendelea kama Shirika la Ndege la Ethiopia. Serikali yao iliwawezesha Ethiopia na waliendelea vizuri, ilivumilia na walijipanga vizuri. Walianza mambo yao ya ndege mwaka 1945, lakini walikuja kupata faida 1990 walikuwa wavumilivu, waliwekeza katika mishahara, matangazo na hadi sasa hivi inajiendesha kibiashara. Tusitegemee ATCL itaanza tu, tayari tupate faida asilimia 100, hapana. Lazima kama sisi Serikali kuiwezesha ili iweze kujiendesha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mafanikio ya Ethiopia yalikuwa na uvumilivu, mkakati na nidhamu. Uvumilivu ulisaidia sana mpaka kufika 1990 ukiangalia ukiangalia kuanzia mwaka 1945, ni kipindi kirefu sana, kwa hiyo, kilihitaji uvumilivu. Nasi tukifanya hivyo, Serikali ikiwawezesha ATCL nina uhakika kabisa tutafika na tutaweza kuendelea vizuri na ATCL. Kwa hiyo, naomba Tanzania tui-support ATCL. Mpaka sasa hivi tumeona inaenda vizuri, ni muda mchache sana lakini imefanya vizuri na wote tumekubali.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuonyeshe uzalendo kwenye ndege zetu. Tumeona kuna ndege ndogo ambazo zinafanya safari kwenye miji mikubwa, kwenye barabara kuu ambazo zingeweza kufanya ndege zetu. Naomba pia Serikali iliangalie hili tumetumia kodi za wananchi. Ndege ndogo zinaweza kupewa trip nyingine kwenda sehemu ambazo hizi ndege zetu za ATCL haziwezi zikafika. Zenyewe zikaenda zikawaachia njia ATCL.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumeona kuna tabia moja kuwa ndege inapokuwa na nguvu kuna baadhi ya ndege zinakuja zinawakwamisha, zinaua kabisa. Tumeona ndege tayari ambazo tayari zilikuwa zinafanya vizuri zimekufa, lakini tusikubali hili kwa ndege zetu ambazo zimenunuliwa kwa kodi ya wananchi. Tumeona ATCL inaweza ikaenda Mwanza labda kwa kiasi fulani lakini ndege nyingine ikaenda ikashusha kabisa. Hao ndio wauaji wakuu wa soko letu, Watanzania tusikubali, tuwe wazalendo wa nchi yetu. Mheshimiwa Waziri naomba uje unijibu wakati unajibu hili la ndege nyingine kuja kutuharibia biashara huku tukijua tunatumia kodi za wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tusipokuwa makini tunaweza tukajikuta ATCL inakufa, tukaishia kwenye madeni yasiyolipika. Kwa hiyo, tuunge mkono juhudi za Mheshimiwa Rais na nia yake nzuri ya kufufua Shirika letu la ndege ili lije kufanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie na uwanja wangu wa Ndege wa Arusha Airport. Kiwanja cha Ndege cha Arusha Airport, njia ya kurukia ni fupi, hali inayopelekea ndege za kati na kubwa kushindwa kutua, ikiwemo ATCL, inashindwa kuruka. Kwa hiyo, inabidi wakatize trip za kwenda Arusha. Ukizingatia Arusha ni Jiji lenye biashara, Jiji la utalii, ni kitovu cha utalii ambapo tungeweza kuiingizia Serikali mapato mengi sana kutokana na utalii. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wakati ananijibu, naomba aniambie ana mpango gani na Kiwanja cha Ndege cha Kisongo cha Arusha ili nasi wana-Arusha tuweze kupata hizo ndege tuweze kuiingizia Serikali mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naomba Waziri aniambie ameandaa kiasi gani cha uwekezaji kama mtaji na rasilimali watu kuwekeza kwa ajili ya ATCL iweze kujiendesha yenyewe kibiashara? Siyo kuwekeza tu kwenye ndege tukasahau kuwa inahitaji na yenyewe kujiwekeza? Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Kwanza kabisa naomba sana niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais John Pombe Magufuli kwa kuendelea kutimiza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kuwa tunajenga Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikiongea kila siku hapa kuhusu Kiwanda cha General Tyre cha Arusha nimeona kimetengewa pesa ili kianze, lakini ninachoomba je, tumejipangaje kuhusu viwanda vingine vinavyotengeneza matairi hasa vya nje? Je, Kiwanda cha General Tyre tumejipangaje ili kifanye biashara vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nilikuwa naomba reli ya Tanga – Arusha mpaka Moshi. Reli hii itasaidia sana katika usafirishaji wa matairi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Arusha kuna viwanda vingi tu, kuna Kiwanda cha Lodhia Plastic. Kiwanda hiki kimeajiri Watanzania 700; ni kiwanda cha mabomba na ma-sim tank. Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja tulitembelea kiwanda hiki, ni kiwanda chenye ubora wa hali ya juu na aliagiza baadhi ya ofisi zetu za Serikali zitumie kiwanda hiki, lakini ma-engineer wa Serikali wamekuwa wakikwamisha kiwanda hiki. Wamekuwa wakiagiza mabomba nje ya Arusha, wamekuwa wakiagiza mabomba Dar es Salaam ambapo kwanza ni gharama kubwa sana, wamekuwa wakiagiza wakandarasi wanunue mabomba kwenye viwanda fulani, sijui kuna nini (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizo figisu figisu hizo nahisi kuna rushwa. Tumekuwa tunakwamisha Watanzania ambao wanajitokeza kuendeleza viwanda vyao kutimiza kauli ya Rais wetu Tanzania yenye viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aangalie hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu alishatoa amri sijui kama kuna amri nyingine zaidi ya Waziri Mkuu. Tujue hawa ma-engineer wa Serikali ni kitu gani hasa wanapata mpaka wanatoa amri kwa makandarasi ili waende wakachukue mabomba kutoka kwenye viwanda vya nje ya Arusha, kwa sababu kwanza ni gharama. Tunasema tunabana matumizi matumizi gani tunabana kama ni hivi? Tunahujumu na tunamhujumu Rais wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Arusha tuna Kiwanda cha Gypsum kinaitwa Saint Gabain Lodhia Gypsum. Kiwanda hiki kinatumia makaa ya mawe wanatoa Kiwira, mpaka wafike Arusha wanatumia dola 120 mpaka 130. Kiwanda hiki kimekuwa kinatozwa pesa nyingi tofauti na viwanda vingine. Wamekuwa wananunua makaa ya mawe dola 65 mpaka 70; huku viwanda vingine vimekuwa vinatoa dola 35.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba Waziri aangalie sana, tunazidi kukwamisha jitihada za Rais wetu za kuwainua Watanzania. Pia kiwanda hiki kimeajiri Watanzania 450. Hiki cha plastic tayari Watanzania 250 wameshapunguzwa kwa ajili ya hawa watu ambao wanatuhujumu. Ninaomba sana kwa kweli Mheshimiwa Waziri mimi nitashika shilingi nisipopata jibu la kiwanda hiki cha plastic, nisipopata jibu kiwanda hiki ambacho kinatumia Makaa ya Mawe ya Kiwira. Naomba Mheshimiwa Waziri uje na majibu yanayoeleweka ama sivyo sitakuelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri Mkuu alikuja tulitembelea Kiwanda kimoja cha Hans Paul. Yule ni Mtanzania ana kiwanda, anachukua magari Anaya-design yanakuwa magari ya kubebea taka. Magari yake anauza shilingi milioni 200 mpaka 220. Mheshimiwa Waziri Mkuu mwenyewe aliona alishaanga sana hakutegemea kama watanzania wanaweza wakawa na ujuzi kama huo. Ni magari mazuri na yana ubora wa hali ya juu. Ningeshauri baadhi ya Halmashauri zetu zitembelee zione kuliko uangize magari kwa bei zaidi ya shilingi milioni 500 huku tunaweza tukapata magari yenye ubora wa juu hapa hapa nchini kwa shilingi milioni 220. Naomba sana tulinde viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Arusha tulikuwa na kiwanda kikubwa sana cha dawa kimefungwa mpaka leo na kimefungwa na Tanzania tuna uhaba wa dawa. Kwa nini kisifunguliwe hata kisaidie hata Kanda ya Kaskazini yote?

Naomba sana Mheshimiwa Waziri uje kunijibu na hili kiwanda cha dawa cha Arusha kimefungwa mpaka leo. Naomba sana kiwanda hiki kifunguliwe Serikali ijipange ifungue kiwanda hiki. Tunayosema Tanzania yenye viwanda haitakuwa yenye viwanda bila kutekeleza haya ninayokuambia Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kuna watu ambao walipewa viwanda vilivyokuwa vya Serikali, lakini viwanda vile wameng’oa mashine, viwanda vingi tu havitumiki tena. Tunaomba viwanda hivi mkiweza mvirudishe Serikalini ili vifanye kazi, Watanzania waweze kupata ajira tuweze kutumia na sisi bidhaa zetu. Watu wengi walipwa viwanda lakini wamefanya ma-godown.

Mheshimiwa Naibu Spika, Arusha tunajua ni mkoa ambao unaongoza sana kwa mifugo, ni Mkoa ambao una wafugaji wengi sana. Tunaomba na sisi mtuwekee angalu kiwanda cha ngozi ili tuweze kutumia mifugo yetu na itufaidishe tuweze kutengeza viatu. Ngozi inatengeza vitu vingi sana tunaombasana mtuangalie Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko makubwa sana kwa wafanyabiashara, wanakata tamaa wanashindwa kuendelea, tunakwamisha jitihada za Watanzania. Kuna process ndefu sana katika kupata vibali cha kuanzisha biashara. Wanapitia sehemu nyingi sana mpaka wanakata tamaa. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wasaidie Watanzania wengi, hiki ni kilio cha watu wengi sana. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri narudia tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana mimi leo kweli nitashika shilingi Mheshimiwa Waziri asiponijibu kuhusu Kiwanda cha Plastiki cha Lodhia. Vilevile nilikuwa naomba washirikiane na Waziri wa Maji hata idara zetu za maji mfano kama AUWSA watumie watu ambao wako kwenye mikoa yao maana viwanda ni vizuri, kuna hujuma hapa; na hawa ma-engineer wa Manispaa wa mikoa yetu nilitaka nifahamu wenyewe wana nguvu gani kuliko Mheshimiwa Waziri Mkuu? Kama Mheshimiwa Waziri Mkuu anatoa amri hawaitekelezi wanatuma mabomba wakachukue mabomba Dar es Salaam inawezekana kweli? Wanapatanini? Kwanza gharama ni kubwa; tunasema Serikali yetu tunabana matumizi naomba tusimuangushe Mheshimiwa Rais ana nia nzuri na Watanzania ana nia nzuri na nchi yetu, ana nia nzuri na chama chake ambacho ndiyo anatekeleza Ilani yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina mengi, naunga mkono hoja, lakini Mheshimiwa Waziri nitashika shilingi leo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa jitihada zake za dhati za kutatua mgogoro wa Pori Tengefu la Loliondo. Mgogoro huu ulikuwa ni wa muda mrefu sana, wananchi walikuwa wanachomewa maboma yao, mifugo ilikuwa inateketezwa, lakini sasa wananchi wa Loliondo wanaishi kwa amani. Hii ni kwa sababu tunaona jitihada kubwa sana ya Serikali na najua kabisa kwamba vijiji vitarudi kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Arusha tuna wajasiliamali wadogo wadogo katika soko linaloitwa Masai Market lililopo karibu na CCM Wilaya ya Arusha Mjini. Soko hili lina wajasiliamali wanaofanya biashara za utalii hasa akina mama ndio wengi na tunajua mama ndiyo msingi wa familia. Wafanyabiashara hawa wamekuwa wanapata changamoto kwa sababu baadhi ya watalii wakija wakinunua vitu vyao hususani vinyago wanapata shida kupita airport, wanazuiliwa. Hali hii inaleta mkanganyiko kwa akina mama na tunajua kabisa wanatafuta vipato vyao kihalali kabisa. Naomba Serikali ijaribu kuangalia ni jinsi gani itawasaidia akina mama ili watalii hao wakinunua vinyago hivyo waweze kupita airport bila tatizo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Arusha tumejengewa Kituo cha Polisi cha Kitalii cha Kidiplomasia. Kituo hiki kimejengwa kwa jitihada kubwa za Mkuu wetu wa Mkoa Ndugu Mrisho Gambo na wadau wa utalii (TATO). Hata Mheshimiwa Rais alipokuja alifurahishwa sana na ubunifu huu. Hata hivyo, kituo hiki pamoja na kwamba wadau wamejitahidi lakini tulikuwa tunaomba Serikali japo ituletee hata gari kwa sababu kituo hiki kimeleta heshima kubwa katika Mkoa wetu wa Arusha. Kituo hiki ni kwa ajili ya kutatua changamoto za watalii na wageni wanapopata matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mhifadhi wa Ngorongoro, Ndugu Manongi. Wanasema kwenye ukweli tuongee na mimi naongea ukweli. Ndugu Manongi aliajiriwa tarehe 30/10/2013 akaanza kazi Januari, 2014 alikuta mapato ya Ngorongoro yalikuwa shilingi bilioni 59. Kufikia Juni, 2017 alifikisha mapato shilingi bilioni 104 na Juni mwaka huu anategemea kufikisha mapato ya shilingi bilioni 122, ina maana atakuwa ameongeza mara mbili ya kiasi alichokikuta. Hadi sasa ameshakusanya zaidi za shilingi bilioni 110. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ngorongoro lilikuwa shamba la kuiba yaani watu walikuwa wanaiba, kulikuwa hamna chochote. Huyu Ndugu Manongi nakumbuka alipigwa vita sana, sasa nimegundua kumbe vita ilikuwa kwa sababu ya kubana matumizi kama hivi. Kwa hiyo, naomba sana nichukue nafasi hii kumpongeza Bwana Manongi na naomba aendelee kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa kazi hii kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu huyu Ndugu Manongi kajitahidi kuongeza aina mpya ya utalii, utalii wa miamba ya mabadiliko ya sura ya nchi (Geotourism). Naomba nimpongeze sana. Vilevile ameboresha mapango ya Olduvai Gorge sasa yamekuwa katika mazingira mazuri sana, hata Makamu wa Rais alikuja akazindua. Kama watendaji wengine wangekuwa kweli wanamsaidia Mheshimiwa Rais hivi, kwa kweli Rais wetu angekuwa hana kazi kubwa sana, hongera sana Bwana Manongi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara wa hoteli za middle class wamekuwa wakipata shida sana kwa sababu ya tozo nyingi. Wafanyabiashara hawa wamekuwa wakitoza watu Sh.25,000 hadi Sh.45,000, lakini wanatozwa TALA license USD 4,500, ambayo ni kama milioni 6, hapohapo kuna property tax. Tunajua sasa hivi biashara ni mbaya na ukijumlisha kodi na tozo, wana kodi 56. Wafanyabiashara hawa Waziri alikuja tukakaa kikao, Waziri aliondoa TALA licence, lakini aliondoa kwa kuongea tu hakuweka in writing, kwa hiyo hawa wafanyabiashara wamekuwa wakisumbuliwa sana. Huku wenyewe wanasema Waziri ameiondoa, huko wanapotakiwa watoe wanaambiwa hatuna barua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi Mheshimiwa Waziri namwamini na naamini utendaji wake, naomba sana aweke kwa maandishi ili hawa wafanyabiashara wa middle class hotel waache kusumbuliwa na kama alitoa agizo naomba aliandike. Mheshimiwa Waziri kwa sababu namwamini najua hata hii lunch break anaweza kuandika hiyo barua, kwa sababu wafanyabiashara hawa wamekuwa wakisumbuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wafanyabiashara wa utalii wamekuwa na changamoto kubwa sana, wana kodi nyingi sana ambazo wanatakiwa watoe lakini kodi hizi zinapitia sehemu nyingi sana, wenyewe wako tayari kutoa lakini wanaomba liwekwe dirisha moja. Kwa sababu zimekuwa zinawapotezea muda wao mwingi kutembea huku na huku ili kulipa kodi hizo. Tatizo hili lingeweza kutatuliwa kwa dirisha moja tu. Hii inasaidia pia kuokoa muda na pia usumbufu kwa hawa watu unakuwa umemalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nashauri, Arusha kingejengwa Kituo cha Kuvutia Watalii (Theme Park).

Hii park itasaidia sana kwa sababu tumeona watalii wanakuja Arusha wanaenda mbugani lakini tukiweka kivutio kama hiki, tuweke kumbi za starehe, tuweke hata zoo wale watalii wakija watakuwa wanapata muda wa kukaa Arusha na vilevile na sisi tutachukua hizo dola zao. Kwa sababu watalii wakija wanaenda mbugani, wakitoka mbugani wanaondoka. Tukiwawekea kitu ambacho kitasababisha wale watalii waendelee kukaa pale Arusha itatusaidia sana kuingiza pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Kigwangalla na Naibu wake na uongozi mzima wa Wizara. Tumeona tangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla amechagulia jamani yuko field muda wote anafanya kazi. Tukubali, tukatae wanamsaidia Rais, wanafanya kazi nzuri sana. Hongera Mheshimiwa Waziri, tuko na wewe na tunakuunga mkono. Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla amekuwa msikivu hata ukimwambia issue yoyote anaitatua kwa haraka. Nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri, endelea kuwa na moyo huo huo, endelea kumsaidia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba atakapokuja kujibu, anijibu kuhusu hii barua ambayo aliongea kwa maneno, anatakiwa aweke kwa maandishi na vilevile hizi tozo za hawa wadau wa utalii ambao wanataka liwe dirisha moja. Nakuamini sana Mheshimiwa Waziri najua hii utalitendea haki kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Tumeona alivyokuja Arusha, alijumuika na wadau wengi wa utalii. Vilevile pongezi zangu ziende kwa Mkuu wangu wa Mkoa wa Arusha, tumeona anavyojitahidi kukuza utalii wetu kwa kukutana na wadau mbalimbali na wadau wa utalii sasa hivi wamekuwa wanaongea kitu kimoja hata wakileta tatizo wanalileta kwa umoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nianze kwa kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kulinda rasilimali zetu yakiwemo madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nielekeze mchango wangu moja kwa moja katika Mkoa wa Manyara, Mererani. Naipongeza sana Serikali na Wizara na Jeshi la Ulinzi kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kujenga ukuta wa Mererani. Kwa kweli, vijana wale walikuwa wazalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza Mkuu wa Majeshi kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kumaliza ule ukuta wa Mererani kwa wakati. Ingawa Mheshimiwa Rais aliposema kuwa ule ukuta ujengwe, watu walibeza sana kuwa hautaisha, lakini Jenerali Mabeyo alijitahidi wakamaliza kwa wakati. Naomba niwapongeze sana. Kweli nchi yetu ina watu wazalendo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu tu alipoamua kujenga ukuta wa Mererani alitaka madini yetu tuyauze wenyewe na yatufaidishe Watanzania wenyewe ili tulipe kodi na hizi kodi zinufaishe nchi yetu katija sekta mbalimbali. Kwangu mimi ukuta ni ishara tu ya ngome ya ukuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ukuta huu uwe kumbukumbu, mali zetu ni lazima zitufaidishe sisi wenyewe na sasa mali zetu imetosha kuwanufaisha wageni na Watanzania wachache. Madini yetu yanatakiwa yatunufaishe Watanzania na vizazi vijavyo. Mheshimiwa Rais wetu ana nia hiyo na Watanzania tunamuunga mkono Rais Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa uzalendo huu mkubwa aliouonesha kwa nchi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuta huu wa Mererani unatakiwa uwe kielelezo cha dhuluma iliyodumu tangu mwaka 1967 ambapo madini haya ya tanzanite yaligundulika. Mheshimiwa Rais wetu tumeona alivyoonesha uzalendo kuzungushia ukuta na kuwa mkali na rasilimali hii ya madini hasa haya ya tanzanite. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada kubwa ya Mheshimiwa Rais wetu pamoja na Wizara, lakini nataka kusema hivi, madini bado yanatoroshwa. Madini ya tanzanite bado yanatoroshwa, yanaenda nchi za nje, wanapitia njia mbalimbali. Naamini sana vyombo vya ulinzi na usalama vifanye kazi. Kama tu mimi Mbunge najua kuwa madini ya tanzanite bado yanatoroshwa, nina uhakika kwamba wenyewe wakifuatilia hili watagundua na wawe makini sana na mipaka yetu. Madini ya Tanzanite bado yanapita mipakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kwa hii kazi kubwa, Wizara inavyohangaika na Mheshimiwa Rais wetu, watakaokamatwa wanatorosha madini yetu, naomba wachukuliwe hatua kali sana. Hawawezi wakachezea rasilimali zetu ambazo tumekuwa tunahangaika nazo kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niko Mererani. Tumeona wale Wanaapolo wakiwa wanachimba madini na tunaona wale wamiliki wa migodi wakiwa wanahudumia madini. Hii migodi ya Mererani ni kama bahati nasibu. Mtu anaweza akachimba hata miaka 10 au 20 asipate. Kuna kitu kimoja tulikisikia hata kwenye Kamati yangu nilibisha sana kuwa hawa wamiliki wa migodi wawe wanawalipa mshahara hawa wachimbaji kila mwezi. Kwa kweli, tusijidanganye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara wanatakiwa wafanye uhakika wa hiki kitu, wakiangalie kwa umakini, ni ngumu sana. Kwa sababu hawa wachimbaji unakuta wakati mwingine mpaka wanakopa tu ili kulisha migodi yao ili iweze kutoa mawe na unakuta inakaa hata miaka 20 haijatoa. Nasi tangu tunakua tunaonana na Wanaapolo tunaishi nao mitaani, haijawahi kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tu Wizara iangalie mkakati mzuri wa kuweka ili hata watakapopata waangalie hawa wachimbaji ambao tumezoea kuwaita Wanaapolo wapate malipo yao, kwa sababu, kwa kusema hili la kulipwa kila mwezi tusijidanganye, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja katika Mkoa wangu wa Arusha, Wilaya ya Longido, Kijiji cha Mundarara. Kijiji kile kina wachimbaji wa madini ya aina ya rubi. Wachimbaji hawa wamekuwa wakihangaika muda mrefu sana kujitafutia kipato chao kihalali kabisa, lakini wachimbaji hawa wamekuwa wakipitia changamoto mbalimbali ambapo wana imani kubwa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwamba itatatua kero zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa waliyonayo ni madini haya mara wanapopata wanataka yakatwe na madini haya yakishakatwa thamani yake inapungua. Sasa tunakuwa tunafanya nini? Tunataka tuwasaidie wananchi wetu au tunawaumiza? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikatai kunaweza kukawa kuna sheria, lakini Wizara lazima ikae tuangalie hii sheria, kama inawaumiza wananchi wetu, ibadilishwe, tutunge sheria ambayo inawafaidisha. Kwa sababu tunasema madini yanatakiwa yanufaishe Watanzania na wananchi wetu wote kwa ujumla. Sasa kama haya madini yakikatwa yanaumiza wananchi wetu, yanawaumiza hawa wachimbaji, kwa nini tusiangalie sheria ambayo itawasaidia wachimbaji hawa wa Mundarara ili na wenyewe waweze kuchimba kwa amani na waweze kupata thamani na madini yao ili malengo yao waliyokusudia yatimie? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri, dada yangu Mheshimiwa Angellah Kairuki, kaka yangu Mheshimiwa Doto na Mheshimiwa Nyongo nawaamini, najua kwenye hili mtawatendea haki watu wa Mundarara. Nawaombeni sana mnapokuja, mje na jibu la uhakika ili watu wa Mundarara wajue hatima yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba sana watakapotoa vitalu katika maeneo haya waangalie wazawa ambao ni wananchi wa Longido. Wasije wakawapa wageni tukawasahau wananchi wazawa ambao ndio wapo katika maeneo hayo kila siku. Naomba sana Mheshimiwa Waziri hili suala aliangalie kwa makini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nakushukuru sana, siku ambayo niliuliza swali kuhusu Longido, Mundarara hapa, nashukuru Mawaziri wangu ni wasikivu. Mheshimiwa Nyongo alienda mpaka Mundarara baada tu ya kuuliza lile swali na akakutana na wananchi wa Mundarara. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Manaibu wako kwa kuwa wasikivu kwa wananchi na Wabunge kwa ushauri wetu. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niendelee kuipongeza Wizara ya Nishati na Madini kwa kazi kubwa inayofanya tangu kuanzishwa kwake. Tumeona maduhuli yanazidi kuongezeka. Kwa mfano, mwaka 2017/2018, Wizara ilipangiwa kukusanya shilingi bilioni 194.66 lakini hadi tarehe 31/03/2018 ilikusanya shilingi bilioni 225 sawa na 115.59%. Mafanikio haya yamechangiwa na juhudi mbalimbali ikiwemo kurekebisha Sheria ya Madini ya Mwaka 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipongeze sana Serikali, naomba nimpongeze dada yangu ambaye ni Waziri wa Madini wa kwanza, Mheshimiwa Dada Angellah Kairuki, unafanya kazi sana mwanamke mwenzetu. Naomba tukutie moyo na wanawake wenzako tunaendelea kukutia moyo, piga kazi tuko na wewe na tunakukubali sana. Huna majivuno, unatusikiliza na uko tayari kushaurika na kukosolewa. Piga kazi dada yangu, tuko na wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niwapongeze Manaibu wako Mheshimiwa Nyongo na Mheshimiwa Doto. Vilevile jamani Wizara hii ina viongozi wenye busara sana, wamekuwa pamoja nasi, tunawasumbua muda mwingi na wamekuwa wakitusikiliza na kutatua kero mbalimbali. Kwa kweli, Mheshimiwa Rais hakufanya makosa kuwapa hiyo Wizara, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wangu, aendelee kufanya kazi. Alivyoongea kuhusu ukuta, alivyokuwa anaongea kuhusu madini kuna watu walimdhihaki humu humu ndani, lakini wameshindwa, Watanzania wanamkubali Rais wetu na Ilani ya Chama cha Mapinduzi inaendelea kutekelezwa, tupo na wewe Rais wetu. Piga kazi, sasa hivi matokeo wanayaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na umahiri mkubwa wa CAG nafikiri kuna umuhimu wa viongozi kuzingatia kauli zao hasa kulinda uzalendo wa nchi yetu. CAG amekwenda Marekani matokeo yake anaponda Bunge, anasema Bunge dhaifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi namwambia CAG Bunge siyo dhaifu, Spika wetu siyo dhaifu, kuna mengi sana ya kuongelea mazuri kuhusu Bunge hili. Nilitegemea msomi kama CAG atayaongelea hayo matokeo yake amesema Bunge dhaifu kitu ambacho ni kinyume kabisa ni kwamba CAG ameongea uongo Bunge siyo dhaifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, CAG pamoja na yote hayo tulisema labda aliteleza. Ameitwa na Kamati ya Bunge bado ameendelea kuonyesha jeuri akiendelea kusema ataendelea kuitumia kauli hii. Sasa sisi hatuko tayari kuendelea kuitwa dhaifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, CAG amekuwa akifanya kazi na Kamati ya PAC na LAAC, sidhani kama kuna chochote alifikisha huko kikashindikana matokeo yake ameenda kuongea nje ya nchi, ameshindwa hata kulinda Taifa lake amekwenda kutusema kwenye mataifa ya nje ambapo dunia nzima wamesikia kumbe Bunge dhaifu. Kwa hiyo, kauli hiyo tunaikataa kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile CAG alikuwa na muda alivyoitwa na Kamati kusema basi hata asamehewe matokeo yake ameendelea kurudia kauli hiyo. Amesema ni lugha ya kiuhasibu, mimi sijui kama wahasibu wana lugha ya udhaifu, ametudhalilisha na amelidhalilisha Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana kabisa na Kamati hatuko tayari kufanya kazi na CAG ambaye ameshatudharau na kutuita sisi dhaifu. Naungana na hoja ya Kamati. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Dotto Biteko na Naibu wake Mheshimiwa Stanslaus Nyongo kwa kazi nzuri wanayoifanya. Mheshimiwa Dotto, tunajua mti wenye matunda ndio unaopigwa mawe; hayo mawe endelea kuyapokea, piga kazi kama unavyopiga msaidieni Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tarehe 22 Januari, Mheshimiwa Rais aliitisha kikao cha wadau wa madini wote Tanzania pale Dar es Salaam; na wadau wale walifurahi sana na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa wanyonge kwa kuwajali na kuwaona na kuona umuhimu wao na kuwaita.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa changamoto ambazo wadau wa madini waliziomba kwa Mheshimiwa Rais; changamoto kubwa ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo ilikuwa asilimia 18 na kodi ya zuio asilimia 5. Mheshimiwa Rais aliyapokea na akaahidi atayafanyia kazi. Serikali sikivu ya Awamu ya Tano ilileta Bungeni tarehe 9 Februari kufanya marekebisho Muswada wa Sheria wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) na hii ya zuio la asilimia tano, ilipitishwa na Mheshimiwa Rais alisaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mpaka sasahivi zuio ndilo ambali limepita lakini mpak asasahivi wachimbaji wanateseka. TRA bado wanachaji ongezeko la VAT la asilimia 18, sasa mimi najiuliza, kama Bungeni tulipitisha, Mheshimiwa Rais alisaini, wao ni nani? Najua Waziri wa Fedha ananisikia, jamani hawa wafanyabiashara wa madini wanateseka, na mnawachonganisha na Mheshimiwa Rais, alipitisha na Bunge tulipitisha, nani mwingine zaidi wa kuacha kutekeleza haya maagizo? Waziri wa Fedha unanisikia, Waziri wa Madini unanisikia na leo nashika shilingi kwa sababu Bunge tulishapitisha. Hawa wafanyabiashara wazawa wana mitaji midogo ukilinganisha na wageni ambao hii asilimia 18 ya VAT haiwahusu, inawahusu hawa hawa wafanyabiashara wetu wadogo.

Mheshimiwa Spika, naomba sana Serikali uangalie na Mheshimiwa Rais huko ulipo unisikie, ulichokisaini mpaka sasa hivi wafanyabiashara wa madini hawajatendewa haki. kwa hiyo Mheshimiwa Rais siku ile ni kama siku nzima amekaa na wale wafanyabiashara umepoteza muda kwa sababu hawajatekeleza. Tunaomba watekeleze haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze moja kwa moja mchango wangu katika export permit, kibali cha kusafirisha madini. Sheria ya Madini inatamka kuwa Katibu Mtendaji wa Tume ndiye mwenye mamlaka ya kusaini vibali vya kusafirisha madini. Katibu Mtendaji wa Tume yupo Dodoma. Wafanyabiashara wengi nchini wako sehemu mbalimbali. Inachukua muda mrefu Katibu huyu kuletewa hapa Dodoma mpaka kusaini madini yaweze kusafirishwa nje. Hapa Tanzania inachukua hata wiki ilhali wenzetu Kenya wanachukua dakika 10.

Naomba kila mkoa angeteuliwa mtu ambaye mnamuona anafaa aweze k ufanya hii kazi kuliko kukaa kusubiri huyu Katibu Mtendaji wa Tume, akiwa hayuko, akiumwa, kazi zinasimama. Hivi jamani, hii Serikali ya Awamu ya Tano kuna kitu kama hiki? Kazi zisimame kwa ajili ya mtu mmoja? Haiwezekani! Mheshimiwa Waziri, naomba uliangalie hili, wawepo watu ambao wanaweza kufanya hii kazi, sio mtu mmoja tu wamtegemee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona Wizara ya Mazingira imepiga marufuku mifuko ya plastiki. Nawapongeza sana kwa sababu ni katika suala zima la kuhifadhi mazingira; lakini wafanyabiashara wa madini hasa ya Tanzanite wanasafirisha madini yao kwenda nje kwa mifuko ya aina hii ambayo kama imepigwa marufuku madini haya ambayo yanakuwa yamesafishwa, yameshawekwa katika ubora yataharibika. Kwa hiyo wenyewe bila kutumia mifuko kama hii tutaharibu biashara yao. Naomba, najua hii Serikali ni sikivu na iko radhi kuongea na hawa wafanyabiashara, iangalie ni jinsi gani wao waruhusiwe hata kutumia mifuko ambayo wamekuwa wakitumia bila kuathiri mazingira kwa sababu kwanza mifuko yenyewe inaenda nje haikai hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Arusha kulikuwa na maonesho ya madini tangu mwaka 1992, yalikuwa yanaitwa Arusha Game Fair lakini cha kusikitisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Bahati mbaya dakika tano zimeisha Mheshimiwa Catherine.

MHE. CATHERINE V. M AGIGE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kufanikiwa kudhibiti ujangili katika nchi yetu. Tumeshuhudia Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Dkt. Hamis Kigwangala akizunguka nchi nzima, siku 48 pori kwa pori. Nilifuatilia katika Gazeti la Mwananchi, walifanya tathmini, walisema Mheshimiwa Kigwangala amezunguka kilometa 28,000. Mimi mwenyewe nilikuwa nikiangalia najiuliza huyu mtu ni wa namna gani? Kwa kweli Mheshimiwa Kigwangala anastahili pongezi, amefanya kazi kubwa sana; anamsaidia Mhehsimiwa Rais na vilevile hata Watanzania na sisi wenyewe tunamuona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tembo wanaongezeka kwa wingi, wanaendelea kuzaliana, ujangili umepungua. Zamani ilikuwa hata tembo akifa bahati mbaya, unakuta majangili wameshachukua meno ya tembo lakini sasa hivi tembo akifa tunakuta meno kama yalivyo, ina maana ni Wizara imejitahidi sana kupunguza ujangili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuanzisha Jeshi Usu kwa ajili ya misitu na wanyamapori. Sasa hivi wanyama na misitu yetu ipo salama. Vilevile nawapongeza kwa kuanzisha kikosi kazi kwa ajili ya kudhibiti ujangili na ndiyo maana siku hizi hatusikii tena habari za ujangili kama ilivyokuwa hapo nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya watalii inaendelea kuongezeka kila siku, yaani watalii wanaendelea kumwagika katika nchi yetu; zote hizi ni jitihada za Wizara ya Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Waziri, watendaji wake na taasisi zake mbalimbali. Hivi karibuni hapa tumeshuhudia meli ya watalii 2,500, ndege ya Waisraeli1,000 na Wachina 343, wote hawa wanapokuja katika nchi yetu wanaondoka wanarudi huko, wakisharudi fikiria kila mmoja aliyekuja huku akifika katika nchi yake anawaambia watu wangapi na wanatangaza Tanzania kwa namna ama nyingine; wanatangaza vivutio vyetu kwa namna moja ama nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika Mkoa wangu wa Arusha kwa wafanyabiashara wa hoteli za kitalii. Wafanyabiashara hawa wamekuwa wanatozwa bed night levy kwa siku ambapo wanalipa dola moja na nusu. Nayo haijalishi kwa hoteli ambayo labda inachaji dola 150 au 200 kwa siku, au hata ile hoteli ndogo ambayo inachaji kwa siku 40,000, wote wanalipa sawa. Kitu hiki kimekuwa kikiwaumiza sana wafanyabiashara wa mahoteli, kwa sababu inawezekanaje mtu ambaye anachaji mtu kulala kwa siku dola 250 na mwingine 40,000 wakalipa sawa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri alikuja Arusha, alikutana na wadau wa utalii walimwambia, lakini kipindi kile nadhani alishindwa kuamua labda kwa sababu tulikuwa hatujaenda kwenye bajeti. Sasa Mheshimiwa Waziri ndiyo wakati muafaka, wafanyabiashara wa utalii wanamwamini sana na wamesema nimfikishie hili na wana imani kubwa na yeye na atalitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali iendelee kuangalia mazingira ya Ziwa Manyara; kina kinapungua na tunajua kuwa Ziwa Manyara lina ndege wazuri sana ambao ni kivutio cha watalii wengi, ndege aina ya flamingo. Kwa hiyo kina hiki kinapopungua ndege watapotea na tutakosa watalii. Naomba sana Serikali iangalie kwa karibu ili tusije tukapata hasara ya kupoteza ndege aina ya flamingo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali iangalie mazingira ya Ngorongoro kwa sababu Ngorongoro magugu yanaharibu mazingira, wanyama wadogowadogo wanakosa chakula, wanakufa. Serikali ifanye utafiti namna ya kukabiliana na changamoto ya mmea vamizi kwenye Hifadhi ya Ngorongoro ambao ni urithi wetu wa dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wangu wa Arusha, eneo la Ngorongoro kuna shule moja ya wasichana ilitakiwa kujengwa katika Kata ya Alaitole, eneo la Isere. Shule hii wananchi wamejitahidi wamekusanya mawe, wamekusanya mchanga, halmashauri imetupa milioni 288, lakini mpaka sasa hivi Ngorongoro hawajatoa kibali cha kujenga shule hii. Akinamama wamekuwa wakilalamika, hata wiki iliyopita waliandamana, akinamama wanataka watoto wao waende shule, lakini hatujajua ni kwa nini wanazuiwa kujenga, mpaka sasa hivi hawajapata kibali kutoka hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mashaka na Mheshimiwa Waziri, vilevile na watu wa Ngorongoro. Naomba ikiwezekana tukutane twende tukasikilize hasa kuna changamoto gani ili tuangalie ni jinsi gani akina mama hawa watasaidiwa watoto wao waende shule. Tunajua Mheshimiwa Rais anasisitiza watoto wasome na akinamama hawa wanataka watoto wao waende shule na ndiyo maana juzi waliandamana kwa uchungu mkubwa sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri alichukue hili na alifanyie kazi ili shule hii iweze kujengwa na watoto wetu waweze kwenda shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri na watendaji wa Wizara yake kwa kazi nzuri sana wanayofanya ya kuhakikisha nchi yetu inanufaika na vivutio vya utalii tulivyonavyo. Nawapongeza sana kwa mkakati wa ku- rebrand nchi yetu kupitia kaulimbiu ya Tanzania Unforgettable. Hili ni jambo zuri na muhimu katika kutangaza nchi yetu na kuingia katika ushindani wa Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, lazima kufanya kazi ya ziada ili kweli kauli hii iwe ya maana na iwe kauli endelevu. Hii ni kuhakikisha kwamba tunapokwenda kila mahali Watanzania wanaitangaza Tanzania Unforgettable; timu zetu za Tanzania zinabeba Tanzania Unforgettable; wasanii wetu wanabeba, hata Mawaziri wetu wanapokwenda kwenye mikutano ya Kimataifa wanaibeba hii Tanzania Unforgettable. Vilevile hii siyo kazi ya Wizara ya Maliasili tu, ila Wizara ya Maliasili ni kama wenyewe wana- coordinate, lakini tunatakiwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaposema hivi inawezekana hata Wabunge wengi hawaelewi maana yake, hata Mawaziri, inawezekana asilimia 90 hawaelewi, wanahitaji kueleweshwa na kufahamishwa ili tunapoongea Tanzania Unforgettable kila mahali iwe ni kwa ajili ya Watanzania wote, siyo Wizara tu, tuitangaze kila mahali. Tanzania Unforgettable ni experience itakayopata watalii au mgeni kutoka kutangaza. Mfano, mgeni anapofika tunaangalia ni jinsi gani mazingira ya immigration wamempokea mgeni, wamemkaribishaje. Hiyo nayo ni Tanzania Unforgettable, akitoka anakwenda kuitangaza Tanzania. Tunaangalia amepokelewaje kwenye hoteli, amepataje usafiri, usalama wa mgeni, akitoka katika njia salama anakwenda kuiongelea vizuri nchi yetu, tunaangalia mambo mengi kuhusiana na hii. Au njia rahisi za mtu hata kufanya biashara Tanzania, vilevile akitoka anakwenda kuiongelea Tanzania vizuri. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kukupongeza, unajitahidi sana pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara. Naomba atakapokuja kujibu anijibu kuhusiana na hii shule, maana akinamama kule wanapata shida, wanafuatilia kuhusiana na hii shule. Vilevile na wafanyabishara wa middle class hotels wa Arusha; naomba anijibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri na timu yake nzima kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja nijielekeze kwenye mchango wangu. Naipongeza Serikali kwa kutenga masoko ya madini karibu nchi nzima. Tumeshuhudia masoko ya madini katika mikoa mbalimbali. Serikali imeshirikiana na Makatibu Tawala wa Mikoa mbalimbali, wametenga masoko ya madini na tumeshuhudia masoko hayo zaidi ya 25 na vituo mbalimbali vya madini, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kanuni za uendeshaji wa masoko haya, tunafahamu kuwa majengo mengi ambayo yana masoko haya ni ya Serikali. Mfano tu ni jengo la National Housing la Dar es Salaam PSSSF ya Arusha na AICC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa kwa wafanyabiashara wa madini ya vito ni kwamba wanalipa VAT asilimia 18 Serikalini. Wanatozo nyingi sana ambazo wanatozwa, lakini wanapokuja kulipa majengo yale ambayo ni ya Serikali, wanapokuja kulipia kodi za majengo, wanalipa 18% ya VAT na bado wanatozo nyingine nyingi ambazo zinaenda huku huku Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais, mama yetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alisema, lazima tutengeneze mazingira rafiki ya biashara. Wafanyabiashara hawa wa madini kwa kweli mazingira haya ambayo wanapitia sasa hivi siyo rafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kuhakikisha hii VAT ya asilimia 18 ambayo wanatozwa kwenye kodi ya majengo, iondolewe kabisa wabaki na kodi nyingine. Kwa sababu zote hizi zinaenda Serikalini. Kwa hiyo, inakuwa kama tunawatoza wafanyabiashara hawa kodi mara nyingi hali ambayo inapeleka wanashindwa kabisa kufanya biashara zao; na inasababisha wafanyabiashara ambao sio waaminifu wanatorosha madini. Kwa hiyo, ukiangalia sisi wenyewe tunatengeneza hali ngumu ya wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu mwingine ni juu ya malipo ya PAYEE kwa wachimbaji wadogo wa Tanzanite. TRA imekuwa inawalazimisha wachimbaji kulipa PAYEE ya shilingi 200,000/= mpaka shilingi 400,000/= kwa wafanyakazi kila mwezi. Kibaya zaidi, hakuna uhalisia wa makadirio ya PAYEE ambayo wanalazimishwa kulipa kwa wafanyakazi kila mwezi. Kibaya zaidi na ni double standard ni wafanyabiashara wa Tanzanite Mererani tu ndio ambao wanalipishwa hii, lakini wafanyabiashara wa dhahabu, almasi hawalipishwi hii PAYEE kwa ajili ya wafanyakazi wao, ni wafanyabiashara wa Mererani tu, kwa hiyo, hii ni double standard.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, TRA watafute njia nzuri ya kutafuta kodi, siyo kuwaonea hawa wafanyabiashara. Wanaweza wakawalipisha hata asilimia moja ya madini yaliyothaminishwa, kuliko hivi ambavyo wanafanyiwa na ni wafanyabiashara walioko Mererani tu, yaani wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite, lakini kwa akina rafiki yangu Mheshimiwa Musukuma hapa Geita na sehemu nyingine nyingi hawalipishwi. Kwa hiyo naiomba Serikali iangalie hiki kitu, inakuwaje na ni kwa sababu gani, wafanyabiashara wa Tanzanite wa Mererani ndiyo wanalipishwa peke yao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mchango wangu nijielekeze kwenye malipo ya fidia ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF). WCF wamekuwa wakitaka wafanyakazi kukatwa, kuna malipo ambayo wanatakiwa walipe ambayo hayaeleweki. Hayaeleweki haya malipo ni ya namna gani, wanakatwa wanavyotaka wao. Sasa naomba Serikali ikae iangalie haya malipo ya WCF yanawekwaje wekwaje! kwa sababu, ili yaweze kuwa na uhalisia kamili na vile vile, ili tutende haki kwa hawa wafanyabiashara na tutende haki kwa hii WCF. Kwa hiyo, ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba wakae waangalie haya malipo yako vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan alisema, kumekuwepo na madini kwenye hifadhi zetu. Hifadhi zetu zinafahamika na akasema madini yachimbwe. Ushauri wangu kwa Serikali, tuwatumie GST - Wakala wa Jiolojia na Utafiti, waende kule kwenye hifadhi zetu maana zote zinajulikana, waangalie sehemu zenye madini. Bila kutumia GST watu wataenda watafanya tu uchimbaji holela, maana hawajui wapi kuna madini wanaenda kwa kukisia, lakini GST wakifanya utafiti tutajua moja kwa moja wapi kuna madini na vile vile itatusaidia kuepukana na uharibifu wa mazingira kwenye mbuga zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, GST kama hawana pesa Wizara, Serikali iwapatie GST pesa, wakafanye utafiti, tujue maeneo haya ya hifadhi, ni wapi kuna madini na wapi hakuna madini ili tuepuke uvamizi. Maana watu wanaweza tu kwa kuwa wameambiwa hifadhi hii ina madini, wakaenda wakavamia bila kuwa na utafiti hasa eneo gani, matokeo yake tukasababisha uharibifu wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie mchango wangu kwa kumpongeza mwanamke wa kwanza kuwa Rais wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassani, nimpongeze sana kwa kuwa Rais mwanamke wa kwanza, wanawake tunajivunia kuwa na Rais mwanamke. Vile vile, nimpongeze Mama Samia kesho anaenda kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi. Naomba nimpongeze sana maana najua tunampa kura zote za ndiyo tukiwemo na sisi wanawake, tuko mstari wa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia nafasi hii kumpongeza mama Samia na nimwambie hatutamwangusha, tunajua utendaji wake wa kazi na tupo naye. Nina imani na haya niliyoyaongea hapa, Wizara itayafanyia kazi, Mheshimiwa Doto Biteko namwamini, najua haya mtayachukua na mtayafanyia kazi kwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Afya inayoongozwa na mwanamke shupavu, jasiri ambaye halali usiku na mchana akihakikisha anamsaidia Mheshimiwa Rais kuboresha huduma za afya na si mwingine bali ni Mheshimiwa Ummy Mwalimu akisaidiana na kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mollel nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Rais Samia kwa kutoa fedha nyingi katika huduma ya afya ikiwemo afya ya wakinamama wajawazito na watoto. Vilevile tunaona hii Royal Tour pia fedha nyingi zitakazopatikana zitaenda katika huduma ya afya na kwenye kuboresha pia afya ya wamama wajawazito na watoto. Wanawake wa Arusha tunampongeza sana Mheshimiwa Rais Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia kwa kutoa fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa hospitali za rufaa za mikoa. Sisi wa Mkoa wa Arusha tunaomba hospitali yetu ya Mkoa ya Mount Meru iboreshwe ili iweze kuwatibu wananchi pamoja na watalii sambamba na uboreshaji wa hospitali hii tulikuwa tunaomba Madaktari Bingwa katika fani mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kufahamu ni kiasi gani cha pesa zimetengwa kwa ajili ya uboreshaji wa Hospitali ya Mount Meru ya Mkoa wa Arusha? Mkoa wa Arusha katika Jiji la Arusha tulikuwa tuna kiwanda cha dawa lakini kiwanda kile hakifanyi kazi muda mrefu sana. Kiwanda kile kilikuwa chanzo cha ajira kwa wananchi wa Arusha na mikoa iliyo jirani na Mkoa wetu wa Arusha. Vilevile kilikuwa kinaongeza mapato katika Jiji la Arusha. Tunaomba Serikali mliangalie hili, kiwanda hiki cha dawa cha Arusha kiweze kuanza mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza Rais kwa kupeleka pesa nyingi katika ununuzi wa dawa na vifaatiba. Tumeona mwaka huu zimetolewa Shilingi bilioni 129 MSD, lakini cha kushangaza, kama Mheshimiwa Rais kaidhinisha Shilingi bilioni 129 kwenda MSD, ni kwa nini kuna upungufu wa dawa? Ina maana pale kuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kufanya mabadiliko MSD. Mabadiliko haya yatasaidia sana. Tumeona amemteua Mkurugenzi kijana ambaye tumeambiwa ana uzoefu katika masuala mazima ya dawa. Nina imani kabisa mabadiliko haya yataleta tija katika upatikanaji wa dawa na vifaatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumeona mjumbe wa bodi ni mwanamke. Jamani, tunaona mfano, alipo mwanamke haliharibiki neno. Mmeona mama Rais wetu ni mwanamke, mmeona wafanyakazi sasa hivi wanacheka, huyo ni Rais mwanamke. Kwa hiyo, Mwenyekiti wa Bodi kwa sababu ni mwanamke, waziri naye ni mwanamke, najua kabisa mambo yatakuwa mazuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri tunaomba sana mkajipange, Rais ameshatoa mwelekeao, miezi mitatu minne inawatosha kabisa kujipanga kuhakikisha wananchi wanapata dawa. Hatutaki tena kusikia sababu sababu, tunachotaka wananchi wapate dawa na vifaatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna upungufu wa madaktari. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais, katoa ajira, wameajiriwa katika Sekta ya Afya wafanyakazi wengi, lakini hawatoshi. Tunaomba atoe ajira zaidi kwa wauguzi na wakunga ili wananchi wasipate changamoto tena. Vilevile tumekuwa tukisikia changamoto katika Hospitali za Serikali juu ya huduma. Wizara ya Afya tunaomba mliangalie hili mhakikishe changamoto hizi zinafikia ukomo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais, vilevile tunashukuru Wizara nzima ya Afya, Katibu Mkuu, Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Dkt. Mollel, mnafanya kazi kubwa sana. Tunaomba changamoto hizi ndogo ndogo tunajua haziwashindi. Afya ndiyo kila kitu, tunawaamini, tunaomba mfanye kazi mwendelee kuchapa kazi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ummy Rais amekuamini na hujawahi kumwaibisha Rais. Tunaomba dada yangu Mheshimiwa Ummy ufanye kazi kwa bidii, tuna imani kubwa na nyie, tuna imani kubwa na Naibu Waziri, Katibu Mkuu; Mkurugenzi mpya wa MSD, na wewe na Mwenyekiti wa Bodi. Hatutaki tena kusikia changamoto za dawa na vifaatiba.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Nianze kwa kumpongeza Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ambapo amekuwa Rais wa mfano ndani ya nchi na nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Profesa Mbarawa amekuwa ni Waziri msikivu, mchapakazi na mnyenyekevu pamoja na timu yake. Naomba moja kwa moja nijielekeze katika mchango wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi naweza kusema ni moyo wa uchumi katika nchi yetu. Hatuwezi kukuza uchumi wa nchi kama miundombinu ya usafirishaji wa watu na bidhaa ni mibovu. Duniani kote katika biashara wanategemea zaidi ya asilimia 98 mawasiliano ya usafirishaji wa bidhaa kwa anga, barabara yaani nchi kavu, majini yaani meli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kuongelea bandari yetu. Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari kwa mujibu wa Sheria Namba 7 ya Mwaka 2019 inaruhusu ushirikishwaji wa sekta binafsi katika shughuli za utendaji wa bandari tangu mwaka 2000 kimkataba. Ushauri wangu kwa Serikali, naishauri Serikali iingie mkataba na kampuni yenye uwezo, ili kuongeza ufanisi, tija na mapato kwa Serikali, ili kuepusha hasara kwa wafanyabiashara na ucheleweshaji wa mizigo yao, ma-container huko bandarini na kwenye kupakua mizigo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bandari ya Dar-es-Salaam ina changamoto nyingi sana, naweza nikazitaja chache; baadhi ya changamoto ni haina viwango vya tija kwa huduma za bandari, mifumo ya TEHAMA haisomani, idadi ndogo ya miundombinu ya kuendesha bandari. Vilevile Bandari ya Dar-es-Salaam imefikia ukomo kuhudumia shehena kubwa za mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia wenzetu, mfano majirani zetu Kenya, Bandari ya Mombasa au Durban South Africa, wanafanya kazi vizuri sana, lakini Bandari ya Dar-es-Salaam ni sawasawa mfano unachukua kirikuu hapa unakipeleka kuchukua magunia ya mahindi Soko la Kimataifa la Kibaigwa huku mpinzani wako anaenda na semi-trailer kuchukua yale magunia. Kweli hiyo inawezekana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile imekuwa kero sana kwa wafanyabiashara, tumeona hata huu mgomo wa juzi Kariakoo. Vilevile bandari hii imekuwa inasababisha uchelewashaji huu, wafanyabiashara wanasubiri ma-container yao kuyatoa wiki tatu, mwezi, wengine mpaka miezi miwili, hali inayosababisha mitaji ya wafanyabiashara inakata, hali ya maisha inapanda kuanzia kwa wafanyabiashara wa juu mpaka wa chini, bidhaa zinapanda, imekuwa shida tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliambiwa kuwa bandari ukitoa mzigo Korea mpaka Dubai unatumia Dola 500 tu, lakini ukitoa Dubai mpaka hapa ni zaidi ya Dola 4,000 na hapa ni karibu, tubadilike. Sasa ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Waziri, leo hii kwa kweli, shilingi yake itakuwa halali yangu. Nataka kufahamu kwa nini Serikali inasuasua kuruhusu sekta binafsi kushiriki katika uendeshaji wa bandari? Kesho Mheshimiwa Waziri anapokuja kuhitimisha, shilingi yake ni halali yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja katika barabara. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais ametenga zaidi ya shilingi trilioni tatu kwa ajili ya kuunganisha barabara katika mikoa saba. Pamoja na Mkoa wangu wa Arusha zimeguswa barabara nyingi sana, lakini kuna kipande ambacho Makamu wa Rais juzi ameenda kuzindua Waso mpaka Sale, lakini hiki cha Sale mpaka Mto wa Mbu naomba barabara hii ijengwe kwa haraka sana. Wananchi wanaotoka Loliondo kule wamekuwa wakipata shida sana, wanakaa njiani hata siku tatu vilevile lile ni eneo kwa ajili ya watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona mama anatangaza Royal Tour, lakini pia na hizi barabara nazo tuangalie tuzipe kipaumbele. Barabara ya Sale mpaka Mto wa Mbu naomba Mheshimiwa Waziri aipe kipaumbele sana barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije moja kwa moja upande wa reli. Naipongeza miradi ya ujenzi wa reli za kisasa, SGR, lakini kinachonisikitisha Lot 1 na Lot 2 kwa nini mpaka sasa hivi hazijakamilika? Kadogosa tunamwamini utendaji wake, tunajua ni mtendaji mzuri sana, lakini hapa tatizo ni nini? Watanzania wana hamu na reli yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nashauri, reli hii itakapokamilika, naomba waalikwe sekta binafsi nao ikiwezekana waendeshe reli hii. Serikali imeshaweka nguvu zake kwenye miundombinu, lakini itakapokuja sekta binafsi itasaidia ushindani wa kibiashara, pia kukuza mnyororo wa ajira, pia kuongeza ushindani hatimaye ubora wa kukuza kipato kwa mtu mmoja mmoja na pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kupongeza Air Tanzania. Tumeona Rais mwanamke, tumeona kuna marubani pale wanang’aa wanawake. Nimemwona Captain Hilda Ringo, Captain Salha na wengine. Tumeona ma-air hostess wamependeza kweli, wana kiwango cha kimataifa. Niwapongeze sana, wapige kazi waendelee kuiletea nchi yetu sifa, waendelee kuhudumia vizuri. Tunajua na wenyewe wanapokea wageni mbalimbali wakiwemo na watalii, waendelee kutangaza nchi yetu, wafanye kazi, wamependeza sana na ni warembo kiwango cha kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwa kumpongeza Waziri kaka yangu January kwa kazi kubwa unayoifanya pamoja na timu yako nzima pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Rais hakukosea kukupa hii Wizara unaimudu na unaiweza chapa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuanzisha mpango wa kuwa na hifadhi ya kimkakati ya mafuta na kuhakikisha kwamba TPDC inawezeshwa kushiriki katika biashara ya mafuta kupitia kampuni yake tanzu ya TAN OIL ili kuwezesha upatikanaji wa mafuta nchini. Ieleweke kwamba TPDC haifanyi biashara hii yenyewe inafanya usimamizi inayofanya biashara hii ni TAN OIL. Hii ni hatua nzuri sana niwapongeze, tumeona nchi za wenzetu kama Saudi Arabia, Algeria na Falme za Kiarabu wanatumia makampuni katika mataifa yao katika biashara hii. Niwapongeze sana Serikali niipongeze Wizara na Waziri na timu yako yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa kutenga Shilingi Bilioni 500 kwa kuboresha grid ya Taifa, pesa hizi zitasaidia upatikanaji wa umeme na kupunguza tatizo la umeme. Tunajua umeme ni uchumi, umeme ni kila kitu tunajua Bilioni hizi 500 zitasaidia sana. Sambamba na kupongeza Serikali naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mtendaji Mkuu wa Tanesco Ndugu Maharage Chande anafanyakazi kubwa sana tunaiona na tupo pamoja naye tunamuomba endelea kufanyakazi kuhakikisha changamoto hii ya umeme kwa wananchi inapungua kama siyo kuisha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kutenga Shilingi Bilioni 140 kwa ajili ya kuendelea kusambaza miradi ya umeme vijijini na pia kwa ajili ya kuongeza kusambaza umeme katika vitongoji. Changamoto ya umeme katika vijiji bado ipo kwa baadhi, mimi mwenyewe katika Mkoa wangu wa Arusha katika vijiji vya Wilaya ya Longido, Karatu, Arusha Mjini, Ngorongoro, Arumeru, Meru, kote huko bado kuna changamoto ya baadhi ya vijiji kukosa umeme. Mheshimiwa Waziri nilikuletea list ya vijiji vyangu na uhakika kabisa uliniahidi vijiji vyangu vya katika Mkoa wa Arusha ambavyo havina umeme vyenye changamoto vitapata mpaka vitongoji. Kwa hiyo tunasubiri wananchi wa Arusha umeme huo uweze kutufikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutenga Shilingi Bilioni Moja katika mradi wa kuhamasisha matumizi endelevu ya nishati safi. TUNAJUA 20% ya wagonjwa wanaosumbuliwa na mfumo wa upumuaji unatokana na matumizi ya kuni, tunaimani kabisa mradi huu utasaidia sana hasa akinamama ambao wengi ndiyo tunahangaika katika kupika kwa kutumia kuni. Tunajua Mheshimiwa Waziri wewe ni mdau mkubwa wa mazingira ulikuwa katika Wizara ya Mazingira, Tanzania tulikuwa tumeshazoea mifuko ya plastic uliacha alama ulihakikisha Tanzania sasa hivi mifuko ya plastic hakuna tumeisahau kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukutia moyo Mheshimiwa Waziri najua wewe ni kijana mchapakazi, hakuna sehemu ambayo unapita huachi alama, kila sehemu unaacha alama na tunayo imani kabisa utaacha alama kubwa sana katika Wizara hii tuna imani na wewe, Watanzania tuna imani na wewe, chapa kazi tuna imani na Naibu wako pia Makatibu Wakuu na wote katika Wizara yako timu yako nzima tuna imani na ninyi chapeni kazi wananchi wana mategemeo makubwa sana na ninyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna imani sana na Mheshimiwa Waziri, Rais alimteua January hakufanya makosa kwa sababu tumeanza kuona, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini, tumeona kazi kubwa inayofanywa na Wizara pamoja na Watendaji wote wa Wizara hii, naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)