Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Bernadeta Kasabago Mushashu (34 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri pamoja na Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Antony Mavunde kwa kazi nzuri wanayofanya katika shughuli zao za kumsaidia Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Magufuli pamoja na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kazi nzuri mnayofanya. Ni mwaka mmoja tu tangu mmeingia madarakani lakini mambo mnayofanya ni mazuri sana, uchumi wa nchi hii umeendelea kuwa mzuri hadi sasa hivi viashiria vyote vya uchumi vinaonekana kwamba tunafanya vizuri sana kwenye uchumi. Pato la Taifa limeendelea kukua hadi sasa hivi linaendelea kukua kwa asilimia saba na mmeweza kuu-contain mfumuko wa bei ukaendelea kukaa kwenye tarakimu moja. Vilevile ni furaha ilioje niliposikia kwamba Tanzania iko kati ya nchi sita the best in Africa ambao uchumi wao unakuwa kwa kiasi
kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo mengi ya kujivunia, tumeambiwa TRA sasa hivi makusanyo yameongezeka kutoka kwenye shilingi bilioni 850 mpaka kwenye shilingi trilioni 1.2 ndiyo maana mmeweza kuyafanya mambo makubwa kama kununua ndege. Anayependa apende, asiyetaka
asitake lakini makubwa yanafanyika ndani ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Mmeweza kuwa mnapeleka shilingi bilioni 18.77 kwenye shule kwa ajili ya elimu bure kila mwezi, hongereni sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri Mkuu amezungumzia kwamba mabenki yako salama, mitaji na ukwasi upo wa kutosha. Hapa nina wasiwasi kidogo kwa sababu tukienda kule chini, tukienda mijini na vijijini tunaona kwamba mabenki ya biashara
yamepunguza kutoa mikopo. Tunahamasisha wajasiriamali wengi wajitokeze wafanye shughuli mbalimbali, wafanye shughuli za kilimo, biashara ndogo ndogo, tunahamasisha wananchi waanzishe viwanda vidogo na vikubwa, hivi kama mabenki hayatoi mikopo hawa mitaji watapata wapi? Niombe Mheshimiwa Waziri Mkuu atusaidie ili Serikali sasa iweke mpango wa makusudi wa kuziwezesha hizi benki ili zianze kutoa mikopo kama walivyokuwa wanatoa kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wadogo waliopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitajikita kwenye suala la kahawa. Kahawa ni zao la muhimu sana katika nchi yetu ya Tanzania, lakini lina umuhimu wa pekee kwa sababu tunaliuza nje linatuletea fedha za kigeni. Bei ya kahawa imeendelea kuwa chini kiasi ambacho inakatisha tamaa na ukilinganisha bei ya kahawa ya Tanzania na nchi jirani ya Uganda unakuta bei ya kahawa ya Uganda iko juu pamoja na kwamba nchi hizi zimepakana, ndiyo kitu kinachoshawishi watu wauze kahawa ya magendo kuitoa Tanzania kuipeleka Uganda. Bei ya kahawa kuwa chini ni kwa sababu bei ya kahawa ya Tanzania imegubikwa na tozo nyingi, ada nyingi, kodi nyingi. Wataalam wanasema hizi kodi na tozo zinafikia hadi 26. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, kuna kodi na tozo za zimamoto, OSHA, land rent, crop cess pamoja na kwamba sheria inasema crop cess inaweza kuwa kati ya asilimia tatu mpaka tano, sisi halmashauri zinatoza maximum, five percent. Kuna income tax, cooperate tax, VAT kwenye inputs zote zinazoingaia kwenye kahawa, research cess, Coffee Development Fund ambapo hela zinakatwa kwenye kila kilo, lakini sijawahi kuona huu mfuko unakwenda kumuendeleza au kuendeleza kilimo cha kahawa. Kuna labour charge, service levy, property tax, coffee bags duties, coffee industry licence et cetera mpaka zinafika 26.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tozo hizi ziko kwenye ngazi mbalimbali za uzalishaji pamoja na pale wanapouza nje. Ukienda pale mkulima anapouza kahawa kwenye chama cha msingi, kwenye chama kikuu cha ushirika, kule kwenye mnada Moshi ambapo wana-export kahawa kote kuna tozo kila mahali, lakini mzigo mzima anaubeba mkulima. Tozo hizi ndiyo zinasababisha bei ya kahawa inakuwa chini sana. Kwa msimu huu Mheshimiwa Waziri Mkuu, bei ya kahawa kwa Mkoa wa Kagera ni shilingi1,300, mtu anatunza ule mbuni kwa miezi tisa anapalilia, anakatia na kadhalika lakini anakuja kuishia kupata kati ya shilingi 1,100 na shilingi 1,300.
Mheshimiwa Mwenyekti, tukijilinganisha na nchi jirani ambazo ni washindani wetu katika hili zao la kahawa kama Ethiopia wao wanakata 0.04% kama exchange rate sale price, Uganda wanakatwa 1% export levy, Kenya wanakata 3% tu kwa ajili ya cess, lakini Tanzania tuna different cess’s, licence fees, taxes na tozo mbalimbali zinazofikia zaidi ya 26 na kuifanya hiyo bei iwe chini sana na kuwafanya wakulima wa
kahawa wakate tamaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu amefanya mambo mazuri sana kwenye korosho, tumemuona. Ameweza kuifanya bei ya korosho ikapanda kutoka kwenye kilo moja shilingi 1,200 mpaka shilingi 3,800. Tumuombe chondechonde, mimi kama mwakilishi wa wakulima wa Mkoa wa Kagera na nyuma yangu wakiwa Wabunge wote wa Mkoa wa Kagera, tunamuomba hebu aangalie kwenye hili zao la kahawa, watu wamelia ni kilio cha siku nyingi. Hebu aangalie tunatoa ada, tozo na fees gani ili kumwezesha huyu mkulima na yeye mwenyewe aweze kufaidi jasho lake aweze kupata bei ya juu ili angalau kilo moja isiteremke chini ya shilingi 3,000. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati namalizia, unakumbuka kwamba watu wa Mkoa wa Kagera na Mwanza wanafanya biashara na Uganda kwa kupitia Ziwa Victoria. Meli ya Mv Bukoba ilizama, Victoria imezeeka inakarabatiwa kila kukicha lakini wafanyabiashara wanapata matatizo kwa sababu ili waweze kupeleka mazao yale ina… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati nzima na Kamati ya UKIMWI kwa kazi nzuri waliyofanya ya kuchambua taarifa za utekelezaji wa Wizara mbalimbali na kuweza kuyaleta mapendekezo mbalimbali. Nasema hongera sana, nami naunga mkono hoja mapendekezo yaliyoletwa mbele ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na afya, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa utendaji mzuri sana, wamefanya mambo makubwa sana kwenye upande wa afya. Wote tumeshuhudia operations kubwa sana zinazofanywa kwenye Hospitali ya Mifupa ya MOI, wote tumeshuhudia operation za kileo zinazofanyika kwenye Hospitali ya Moyo ya Jakaya Kikwete, wote tumeshuhudia hata upandikizaji wa figo sasa hivi unaweza kufanyika Tanzania na watu wanatoka nchi za jirani kuja Tanzania kupatiwa huduma hizo. Kwa hiyo, nasema hongera sana kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ugonjwa wa cancer. Ugonjwa wa cancer ni ugonjwa wa ambao umesambaa sana, sasa hivi watu wengi wanaugua ugonjwa wa huu. Kuna cancer ya damu, ubongo, tezi dume, mlango wa kizazi, cancer matiti; kwa hiyo, cancer ziko za aina nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mtu aweze kugundulika kabisa ana cancer, iwe confirmed, anapaswa afanyiwe vipimo vingi ikiwemo na CT-Scan. Unakuta gharama ya vipimo hivyo hasa kwenye Hospitali ya Bugando ambayo kwa Mkoa wa Kagera tunatumia hiyo, unakuta vipimo vina- cost kati ya shilingi 500,000 mpaka shilingi 600,000 kuweza kugundua kama huyu ana cancer kweli au hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda sasa kwenye matibabu labda amewekewa chemo, dose moja ni kati ya shilingi 600,000 mpaka shilingi 700,000. Je, hawa Watanzania tunaowajua na uwezo wao mdogo waliokuwa nao, ni wangapi wanaweza ku-afford kulipa hizo hela zote kusudi wagonjwa wao waweze kupata matibabu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwa Serikali yangu sikivu na Mheshimiwa Waziri kwamba kwa ugonjwa huu wa cancer na kwa wingi na ukubwa wa tatizo lilivyojitokeza, Serikali ingeweka ruzuku kwenye dawa za ugonjwa wa cancer kusudi dawa hizi ziendelee kutolewa bure katika hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa Wizara imefanya kazi nzuri sana kwenye Hospitali za Rufaa kama Muhimbili na nyingine zote, nilikuwa naomba sasa concentration iende kwenye Hospitali za Mikoa, Hospitali za Wilaya, Vituo vya Afya pamoja na Zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia Mkoa wa Kagera; ukienda mkoa wa Kagera utakuta karibu Wilaya zote hazina Hospitali za Wilaya, sana sana tunadandia kwenye hospitali zile za mission.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Wilaya ya Kyerwa. Wote tunajua kwamba Wilaya Kyerwa ni mpya, hawana kabisa Hospitali ya Wilaya, wanatumia pale Isingiro pamoja na Nkwenda ambapo sana sana zile ni sawasawa na zahanati. Nilikuwa naomba Serikali iwasaidie kwa kuwa ni Wilaya mpya hii, iweze kupata Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pale Manispaa ya Bukoba, tangu mwaka 2013 wanajenga Hospitali ya Wilaya. Wameshindwa kwa sababu huu ni mradi mkubwa, kwa bajeti za Halmashauri hawawezi kuukamilisha. Nilikuwa naomba Serikali isaidie kukamilisha Hospitali ya Wilaya ya Manispaa ya Bukoba ikiwemo vilevile na Hospitali ya Wilaya ya Muleba. Hospitali ya Wilaya ya Muleba wananchi walijitahidi, wamejenga majengo mazuri, ila haijakamilika. Sasa hivi MSD wanapatumia pale, wakiondoka yataendelea kuwa magofu na zile juhudi za wananchi zitaharibika bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itusaidie, kwa kuwa hii ni miradi mikubwa na najua siyo kwa Kagera peke yake, kuna maeneo mengine waendelee kutusaidia kuweza kukamilisha hii miradi kusudi huduma ziweze kutolewa kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunajua kwamba katika Mkoa wa Kagera tulipata tetemeko la ardhi. Tulipata athari nyingi, watu walifariki, taasisi mbalimbali ziliathiriwa na nyumba za watu zimeanguka na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia Kituo cha Afya ambacho kiko katika Wilaya ya Misenyi kinaitwa Kabyaile. Hiki kituo kimejengwa kwa nguvu ya Kamati ya Maafa ambayo ni michango ya wananchi na ya Serikali, ni kituo kizuri sana kimejengwa, hata Rais alishapelekwa kukikagua kile kituo. Pamoja na majengo mazuri, kuna theatre lakini hakuna vifaa, kuna mortuary lakini hakuna mafriji na kuna laundry lakini hakuna vifaa vya kusafishia. Naomba Serikali itusaidie kuweka hivyo vifaa kusudi Kituo cha Afya cha Kabyaile kilicho Ishozi, Misenyi kiweze kuanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Hospitali ya Mkoa wa Kagera ambayo inaitwa Bukoba Government Regional Referral Hospital. Hii ndiyo kimbilio la mkoa mzima. Wilaya zote tunategemea hii hospitali, lakini haina wataalamu, ina Madaktari Bingwa wanne tu ambao ni wa meno, wa watoto pamoja na wa macho. Wanne kati ya Madaktari Bingwa kama 24 wanaotakiwa. Ukienda kwa wauguzi, hao ndio kabisa. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba Serikali kwa hospitali hii ipatiwe wataalamu kusudi iweze kufanya kazi. Hatuna surgeon, hatuna daktari wa mifupa. Wote mnajua accidents za boda boda ni kila siku. Sasa bila kuwa na hawa Madaktari Bingwa inakuwa ni shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hiyo hospitali, kuna wodi ya wazazi ambayo ni ndogo sana. Ina vitanda sita tu na hii ni Referral Hospital ya Mkoa, havitoshi na hakuna theatre. Mwanamke akitoka kule, ana uchungu, akaletwa pale kwenye Regional Hospital, akakuta ile multpurpose theatre ambayo na yenyewe ni ndogo, kuna mtu anafanyiwa operation, inabidi huyu mama amcheleweshe. Kwa hiyo, inabidi huyu mama afe kwa sababu amekuta ile theatre inatumika. Tulikuwa tunaomba basi, katika Hospitali ya Mkoa ijengwe labour ward kubwa ikiwa na theatre yake ili tuweze kupunguza vifo vya mama na mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tukumbuke kwamba Mkoa wa Kagera hatuna mahali pa kukimbilia; ukienda huku ni Uganda, ukienda huku ni Rwanda; ukienda huku ni Burundi; sana sana umkimbize mgonjwa kumpeleka Bugando ambayo iko something like kilometa 500 kutoka Mkoa wa Kagera. Ukitaka kutembea kwa meli ni masaa kama manane mpaka 10 au ukizunguka lile ziwa. Tulikuwa tunaomba ile hospitali ipewe ambulance, kwanza na Mheshimiwa Waziri Mkuu alishakuja akaahidi pale kwamba atatoa ambulance. Namuomba Mheshimiwa Waziri Ummy, hilo alichukue kwamba Hospitali ya Government Regional Hospital waweze kupata ambulance kwa sababu ni mbali sana na Bugando waweze kufanya hizo kazi zinazotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri mnayofanya. Nawapongeza kwa uamuzi wenu wa kuweza kukarabati zile shule kongwe. Wote hapa tumesoma zile shule za zamani, shule kongwe karibu
100. Pia naomba Mheshimiwa Waziri aikumbuke na shule yangu, mimi nilikuwa Mkuu wa Shule pale, lakini ni shule ambayo inasomesha wanafunzi wengi wasichana, Shule ya Rugambwa Sekondari na yenyewe imeanza tangu mwaka 1965 inahitaji ukarabati mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumza juu ya matamko ya Waziri wa Elimu. Mheshimiwa Waziri hivi juzi ametamka kwamba watoto ambao watashindwa kufikia ile alama ya ushindi au pass mark wasikariri madarasa. Sasa hapa mimi nazungumza kama mwalimu. Huyu mwanafunzi asipokariri darasa au huyu mtoto aliyeshindwa kufikia alama ya ufaulu, kwa mfano akapata sifuri kati 100, akapata 10 kati 100, akapata 20 kati ya 100 tunamwambia apande tu darasa, tunakuwa tunamsaidia huyu mtoto au tunamlemaza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kwamba watoto wengine hawataki kusoma. Tukumbuke kuna mahali ambapo walimu hawataki kufanya kazi. Sasa kwa nini huyu mtoto badala ya kumpitisha tu akafika form four akapata division zero, akikariri anakuwaje? Mbona hata humu ndani kuna wengi walikariri na wala hawakuathirika? Napendekeza kwamba watoto wawe wa private au wa government, yeyote ambaye atashindwa kufikia alama ya ufaulu akariri darasa tusije tena tukaanza kukimbizana kuangalia namna ya kufuta zero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu shule za private. Kabla mzazi hajampeleka mtoto private anatafuta mwisho anapata shule moja, anaangalia ile shule ina vigezo gani? Wanataka nini? Discipline ikoje? Ufaulu ukoje? Karo ikoje? Mzazi mwenyewe anachagua kwamba anataka kumpeleka kwenye shule fulani ambapo wengine wanatoza karo kubwa, lakini mzazi anaamua anamtafutia mtoto elimu bora, anampeleka kwenye ile shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba Serikali kama inawezekana, hizi shule za private wangeziacha na alama zao za ufaulu kwa kuwa wazazi hawalazimishwi na wala wanafunzi hawalazimishwi kwenda kwenye hizo shule. Wazazi wanawapeleka kabisa kwa mapenzi yao, wawaache kusudi waweze kuwapeleka kwenye hizo shule na pass mark iendelee kuwa zile zile kama shule watakazokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu leo tunajivunia, naona Wizara tunatangaza kwamba baada ya mtihani wa form four, kati ya shule kumi za kwanza au bora zilizofanya vizuri unakuta most of them ni za private ambao walikuwa wameweka viwango vya ufaulu. Kwa hiyo, nilikuwa naomba nishauri kama Mwalimu kwamba shule za private waziache ziweze kuweka ufaulu wao na hii itasaidaia kuboresha elimu katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. BERNADETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi. Kwanza kabisa naanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa hotuba nzuri, lakini vilevile kwa kazi nzuri wanayofanya ndani ya Wizara yao. Kwa kweli, kazi wanayofanya ni nzuri na inaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Utalii ina jukumu la kutangaza utalii na kutangaza vivutio vilivyo ndani ya Tanzania ili kuweza ku-attract watalii wengi waje. Wamefanya kazi nzuri sana, tumeona matangazo kwenye magazeti, kwenye majarida mbalimbali yaliyo ndani na nje ya nchi, tumeona kwenye mikutano wanatangaza, kwenye michezo wanatangaza, kwenye matamasha wanatangaza kwa kweli, wanafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utangazaji huu umeanza kuzaa matunda ndio maana tunaona sasa makundi mbalimbali ya watalii wanaingia kwa makundi kwa maelfu, kwa mamia, ndani ya Tanzania kuja kuangalia vivutio vilivyo kwetu, lakini vilevile imechangia kwenye pato la Taifa kwa sababu, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ametwambia kwamba, imechangia kwenye pato la Taifa takribani dola bilioni 2.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo kupitia TBC kwa kuweza kuanzisha chaneli ya utalii ambayo inaitwa Safari Chanel, kwa kweli hii ndiyo chaneli yetu ila sasa naomba tuiwezeshe iweze kuonekana hata nje kwa sababu tukiendelea kuiangalia sisi wenyewe, haitatusaidia. Nilikuwa nafikiri tuendelee vilevile kuboresha maudhui ya Safari Chanel ili iweze kuvutia watalii wengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tunaonyesha wanyama, mimea, maua na samaki wanaopatikana Tanzania lakini vilevile tuoneshe na hoteli nzuri za kitalii yaliyo ndani ya Tanzania kusudi yule mtalii sasa aone kwamba loh! Kumbe nikienda Tanzania naenda kulala kwenye hoteli nzuri kama hii, tunazo. Vilevile sisi wenyewe tuna utamaduni, ngoma za kitamaduni za kila mahali, tuiweke kwenye ile chaneli kuongeza ule mvuto wa ile chaneli kusudi watu wapende kuiangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, tuonyeshe ndege kubwa zinazotua ndani Tanzania; tuonyeshe KLM, Quatar Airways, Emirates, British Airways bila kusahau ndege yetu wenyewe ya ATCL kwamba inaweza kwenda ikabeba watalii na kuwaleta hapa, kwa kufanya hivyo basi tutaweza kupanua wigo na watalii watakuja wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kupandisha yaliyokuwa mapori ya akiba ya Biharamulo, Burigi na Kimisi ambayo sasa hivi imekuwa hifadhi inayoitwa BBR na kupandisha Ibanda, Rumanyika na sasa hivi inaitwa Hifadhi ya IR kuwa Hifadhi za Taifa. Kwa sasa mmekata mzizi wa fitina, kwa sababu tulikuwa tunakaa humu Wabunge tunachangia tunasema kwanini inaonekana utalii unakuwa promoted kwenye sehemu moja ya Tanzania ambayo ni kaskazini ilhali vivutio vipo katika sehemu zote? Sasa tunaloona mnaenda kutambua hivi vivutio kuviendeleza na kuendeleza utalii katika Kanda ya Ziwa, tunasema asanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi hizi za BBK na IR zinasambaa kutoka Chato ambayo iko katika Mkoa wa Geita kuja Muleba, Biharamulo, Ngara, Karagwe ambazo zipo katika Mkoa wa Kagera. Je, hifadhi hizi zitaendelea kuitwa kwa majina haya BBK na IR au mna mpango wa kuyapa majina mengine yanayovutia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujio wa hifadhi una manufaa makubwa sana. Kwanza zipo karibu na mipaka, kule kwetu tunapakana na nchi ya Rwanda na zenyewe hifadhi zinapakana na Rwanda. Mnapoongeza ulinzi ndani ya hifadhi hizi ina maana kwamba masuala ya ulinzi na usalama katika hayo maeneo utakuwa umeimarika, watu wataweza kupita kirahisi bila kuogopa kutekwa. Vilevile uoto wa asili utakapoongezeka, uta-attract mvua kubwa itanyesha, ile milima iliyo ndani ya hifadhi ndiyo itakuwa inatiririsha maji kupitia Mto wa Kagera, Mto Mwisa, Msega kuingia kwenye Ziwa Victoria, kitakuwa ni chanzo kizuri cha maji kuingia ndani ya Ziwa Victoria halafu tunavuta tunapeleka Shinyanga, Tabora mpaka Singida kwa hiyo ni manufaa makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutakuwa na mimea mbalimbali, samaki wapo mpaka sasa hivi kwenye maziwa mbalimbali yaliyo ndani ya hifadhi; Burigi, Ngoma, Nyarwamba, Kasinga, Nyamarambe na Victoria yenyewe ambao ni wa aina yake, ni adimu. Kwa hiyo, hii itavutia watu ambao wanaotaka kufanya masomo na utafiti watakuja Mkoa wa Kagera, watakwenda Mkoa wa Geita kwenda kujifunza. Ujio huu wa Hifadhi za Taifa utawapa vijana wetu ajira mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maombi kwa Serikali. Kuna vikundi vya vijana; kwa mfano pale Muleba kuna kikundi cha vijana wanatengeneza vinyago, pale Ngara kuna kikundi cha wakina mama wanatengeneza table mats na vitunga mbalimbali, kuna watu Karagwe kule wanatengeneza vitunga, mikeka pamoja na Misenyi; tunaomba wawezeshwe, wapewe mitaji, wafundishwe ujasiriamali kusudi watengeneze vitu vizuri zaidi vitakavyokuja kuwapendeza hao wajasiamali na waweze kuvinunua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuboreshe miundombinu ya barabara zinazozunguka zile hifadhi pamoja na ndani. Kiwanja cha Ndege cha Chato pale, Kiwanja cha ndege cha Bukoba Mjini viendelee kuboreshwa, viwekewe taa kusudi sasa watalii wanaoingia kupitia Uganda, Rwanda na Burundi waweze kutua wakati wowote usiku na mchana na kufanya utalii ndani ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuendelee kuwavutia wawekezaji; hii ni fursa kwa watu wa Mkoa wa Kagera na Mkoa wa Geita, tuone sasa hapa kuna fursa ya uwekezaji, twende tujenge hoteli, tutengeneze zile fukwe zipendeze, tuandae hoteli na mahali pa kulala watalii hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa ya Kagera na Geita ina urithi mkubwa wa historia ya Machifu Abakama, Ebikale; tunachoomba ni kwamba sasa twende tuyatambue maeneo haya yaendelezwe, inaweza ikawa kivutio kimoja wapo cha utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi kubwa ninaloomba, kwenye vijiji hivi na kata zilizokuwa zinazozunguka, hizi sasa ambazo zitakuwa hifadhi, watu hawa wamezoea kuingia kwenye hifadhi kukata miti kwa ajili ya kuni, kutengeneza mkaa na kuwinda, kuna haja ya kwenda kufanya mafunzo na ushawishi wa kutosha ili watu hawa waweze kuelewa umuhimu wa uhifadhi na hifadhi hizi. Mkishafanya hivi ina maana kwamba hawa watu wenyewe sasa ndiyo watakuja kuwa walinzi namba moja ya hifadhi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Wizara, TANAPA, Ngorongoro Conservation Authority, TAWA, TFC na wadau wengine kwa kudhibiti ujangili. Wanyamapori walikuwa wanatoroshwa lakini sasa hivi hali imetulia, nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tembo ni rasilimali ambayo tumepewa na Mwenyezi Mungu, inabidi tuitunze kwa ajili ya vizazi vijavyo lakini na kwa ajili ya dunia nzima. Mnamo mwaka 2009 inasemekana ndani ya Tanzania kulikuwa na tembo takriban 110,000 lakini wakaendelea kuuwawa kikatili na ujangiri na nini na kutoroshwa, ilipofika mwaka 2014 tulikuwa na tembo 43,000 tu kwa hiyo asilimia 60 yote walishauwawa. Lakini nawapongeza sana Wizara, Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri mmefanya kazi nzuri, mikakati mliyoweka na ulinzi mlioweka, sasa hivi tembo wameanza kuongezeka na tunaona data zinasema hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo linalojitokeza sasa hivi, tembo hawa wanahama kutoka kwenye makazi yao, wanakwenda kwenye makazi ya binadamu, wanafanya uharibifu kubwa, wanaharibu mazao ya wananchi lakini wakati mwingine wanaua hao wananchi. Nilikuwa napenda kujua je, Serikali imefanya utafiti kujua kwa nini hili tatizo ndiyo linajitokeza? Kwa nini tembo wameamua kuhama kutoka kwenye maeneo yao wanakwenda kwenye maeneo ya binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, mtu akiharibiwa mazao yake au akauwawa na tembo, fidia inasemaje? Mheshimiwa Waziri nilikuwa naomba ukija kuhitimisha utueleze. Vilevile Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba haya mambo sasa hayajitokezi tena, tembo wakae hukohuko kwenye mbuga/mapori kusudi wasiwaingilie binadamu, binadamu waendelee kufanya kazi zao? Sasa hivi ukiona sehemu mbalimbali wanaonesha kwamba hata watoto wanaogopa kwenda shule kwa sababu ya hawa tembo wanaohama na kuwafuata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nasema Wizara hii ina majukumu makubwa sana, inabidi iongezewe bajeti ili waweze kuboresha utalii na utalii utaweza kutuletea Pato kubwa la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti hii. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Philip Mpango, nampongeza na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa kazi nzuri na kwa bajeti nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaposikia hapa tunakuja tunatamba kwamba kuna mafanikio makubwa ndani ya Sekta ya Afya, tumepata mafanikio makubwa ndani ya elimu, tumeweza kutengezea miundombinu mikubwa ya barabara, ndege, ni kwa sababu Wizara ya Fedha inafanya kazi nzuri. Wameweza kukusanya kodi, wametafuta fedha wakaweza kusimamia, nafikiri kule hakuna mchwa na miradi yote ikaweza kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hii bajeti ni nzuri kwa sababu inalenga wananchi na inalenga maendeleo ya wananchi. Vilevile inalenga kuboresha mazingira ya kufanyia biashara na namna ya kuwashawishi wawekezaji waweze kuja katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Waziri kwa kuweza kuhakikisha kwamba bajeti yake inaondoa sasa tozo zaidi ya 54 ambazo zilikuwa ni kero kwa wafanyabiashara. Nikitoa mifano tu; mnakumbuka hapa wakulima walikuwa wanahangaika wanashindwa kuuza karanga zao, wanashindwa kuuza mahindi kwa sababu yanaingiliwa na sumu kuvu, lakini sasa hivi kwa kuondoa VAT kwenye vifaa vya kukaushia ina maana kwamba basi wataweza kukausha hayo mazao na kuyauza yakiwa vizuri na yakiuzika vizuri kwenye masoko ya nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile taulo za watoto (baby diapers) ushuru umepungua kutoka asilimia kumi mpaka sifuri, ina maana kwa akina mama wengi ambao wanaendelea kuzaa watakuwa wamewapunguzia matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mashine za EFD wamezipunguzia ushuru kutoka asilimia 10 mpaka sifuri, kwa maana hiyo wafanyabiashara wengi watapenda kununua hizi EFDs, kwanza zinakusaidia kutunza hata kumbukumbu za biashara yako. Kwa hiyo wamefanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashangaa watu ambao wamesimama hapa wanasema kwamba bajeti hii haijapunguza tozo kwenye mifugo na uvuvi. Naomba waende wakaangalie kwenye hotuba ya Waziri, ukurasa wa 78 na wa 79, zimetolewa tozo zaidi ya 15 kwenye mifugo na uvuvi na zote zina mashiko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa zamani mtu ulikuwa unajichimbia kisima chako nyumbani lakini unatakiwa kulipa ada ya maji ya 100,000; sasa imefutwa. Wanaoanza biashara wamepewa angalau miezi sita waanze kujiandaa tangu unapopewa TIN unakaa miezi sita unaandaa biashara yako ndiyo uanze kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri vilevile katamka kwamba tangu sasa hakuna mfanyabiashara kufungiwa biashara yake kwa sababu labda hajalipa kodi, labda kwa kibali maalum. Kwa hiyo nasema nawashangaa wote wanaosema hii bajeti siyo nzuri, naomba wote tuiunge mkono kwa sababu ni bajeti ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ushuru wa Forodha umeongezwa kwenye bidhaa kutoka kwenye asilimia 25 mpaka 35 kwenye vibiriti, peremende, chokoleti, chewing gum, soseji, hata ushuru wa maji umeongezeka kutoka kwenye asilimia 35 mpaka 60. Nawashangaa ambao wanabeza juhudi hizi za Serikali, hawajaelewa Serikali inataka kutuambia nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaulize Wabunge wenzangu; tuna miti kibao ndani ya Tanzania, kwa nini tuagize njiti za vibiriti, kwa nini tuagize vibiriti kutoka nje? Vilevile tunafuga ng’ombe, kuku, nguruwe; kwa nini tuagize soseji kutoka nje? Tunalima kokoa, tunalima kahawa, tuna maziwa, tuna jibini, tunalima miwa kwa maana hiyo tuna sukari; kwa nini tuagize pipi na chokoleti kutoka nje? Pia tuna unga wa mihogo, tuna unga wa ngano, tuna unga wa mtama, tuna maziwa, tuna mayai; kwa nini tuagize biskuti ambazo tunaona akinamama sasa hivi wanatengeneza kwa kutumia unga wa muhogo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali inachotaka kutuambia kwa kuongeza ushuru kwenye hivi vitu ni kwamba tusiagize hivi vitu kutoka nje. Inajaribu kulinda viwanda vya ndani, inajaribu kuwashawishi Watanzania tuweze kuanzisha hivi viwanda, tutengeneze peremende, biskuti na tutengeneze hizo soseji hapahapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwamba Serikali sasa akinamama hizi biashara wanaziweza, kwa kupitia Mabaraza na Mifuko ya Uwezeshaji wanawake wako kwenye vikundi mbalimbali wawezeshwe, wapewe utaalam, wapewe mitaji, waweze kuanzisha viwanda vidogovidogo, waweze kutengeneza hizi bidhaa ndani, hakuna haja ya kuagiza hizi bidhaa kutoka nje. Kwa hiyo nawapongeza kwa kuongeza huo ushuru wa forodha kwenye hizo bidhaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta Binafsi ni sekta muhimu sana katika kukuza uchumi wa nchi. Kwenye Sekta Binafsi hukohuko ndiko tunapotegemea viwanda tunavyosema vijengwe, vitakuwa hukohuko, hukohuko ndiko tunapotegemea ajira za vijana wetu, hukohuko ndiko Serikali inakotegemea kupata kodi kwenye Sekta Binafsi. Ni jukumu la Serikali kuhakikisha kwamba sasa inawatengenezea mazingira mazuri ili waweze kufanya biashara yao katika mazingira yaliyotulia, wawe na mfumo mzuri wa kodi, sera, sheria na taratibu ziwe ni zile zinaoeleweka lakini zile ambazo hazibadiliki mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Rais wetu ambaye ameweza kuita kikao akakutana na wafanyabiashara akasikiliza kero zao na namshukuru Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake kwa kuona kwamba sasa kero nyingine zimeanza hata kutatuliwa ndani ya bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka Mheshimiwa Rais aliacha agizo pamoja na Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwamba sasa hii mikutano iende ifanyike kwenye ngazi ya kanda. Napendekeza ianze kufanyika kwenye ngazi za mikoa wafanyabiashara waweze kueleza kero zao. Vilevile kwa sababu tunajua kodi lazima walipe ndiyo, lakini lazima wafanye biashara wapate faida na wao walipe kodi. Kwa hiyo waweze kuleta mapendekezo yao ambayo yatasaidia kuboresha mfumo wa kodi ndani ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa Mkoa wa Kagera wanategemea zao la biashara ambalo ni kahawa na kwa miaka mingi kahawa imekuwa ikichochea na kuleta fedha za kigeni katika Tanzania. Kwa sasa kahawa ilishakuwa tayari imeshakauka, wanayo majumbani, msimu ulishaanza tangu tarehe Mosi, Mei, ni takribani miezi miwili, hakuna kahawa hata moja imeshanunuliwa Mkoa wa Kagera kwa sababu Vyama Vikuu vya Ushirika hawana fedha, Benki ya Kilimo haijatoa hela ya mikopo kwa Vyama vya Ushirika ili waweze kununua hizo kahawa kutoka kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, wasiwasi wangu ni kwamba sasa hawa wakulima wana shida, wanazo kahawa ndani, watashawishika wataanza kuziuza butura, wataanza kufanya magendo wataharibu kazi nzuri ambayo imeshafanywa na Serikali, ikasimamiwa na wakuu wa wilaya wote katika Mkoa wa Kagera pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, kazi ya utokomeza magendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe basi Serikali kwamba Benki ya Kilimo iongezewe mtaji na kwa haraka sana wapeleke hela kwenye Vyama Vikuu vya Ushirika Mkoa wa Kagera ambayo ni Ngara Farmers, KDCU na KCU ili sasa pamoja na kwamba tumeshachelewa miezi miwili, waruhusu kahawa zianze kununulia na mkulima akiuza kahawa anakuta hela iko pale analipwa palepale, kutakuwa hakuna manung’uniko. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri atueleze hizo hela za Benki ya Kilimo kwenda kwenye Vyama Vikuu vya Ushirika Mkoa wa Kagera zitaenda lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nawasilisha kilio cha wazabuni. Wazabuni hawa walitoa huduma ya vyakula katika shule mbalimbali, labda hata katika hospitali na nini, lakini tangu mwaka 2011 leo hii ni mwaka 2019, wengine hawajalipwa kwa maana ya Mkoa wa Kagera, wanadai zaidi ya milioni 600 na kitu, haya ni madeni ya wazabuni ambayo yalishahakikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wazabuni walifanya makosa gani? Walitoa huduma kwa Serikali, na Serikali wale watoto kama ni shuleni wakala, wakaendelea kusoma; hawa wazabuni walikopa hela kutoka kwa watu mbalimbali kwamba labda niamini hela nitaleta, hawakuleta, kwa hiyo hawaaminiki tena. Hawa wazabuni walikopa katika mabenki…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Spika wetu wa Bunge kwa uamuzi wake wa kugombea nafasi ya Urais wa Bunge la Dunia (IPU). Mheshimiwa Tulia Ackson unastahili, unaweza, wote humu ndani tunatambua uwezo wako na tunataka dunia watambue hilo. Tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu, akubariki na akuwezeshe kupata nafasi hiyo ya Urais wa Bunge la Dunia. We wish you all the best. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wote kwa hotuba nzuri ya bajeti lakini pamoja na kazi nzuri inayofanyika katika Wizara hii. Mheshimiwa Mchengerwa nakufahamu sana nikiwa kwenye Kamati ya Huduma nilikuona makali yako ukiwa kwenye Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo na nina uhakika kwa kuwa sasa hivi unaye na Naibu Waziri ambaye ni makini mchapakazi, mnaenda kuipaisha hii Wizara, mnaenda kupaisha hizo sekta ambazo mnazisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza sana kipenzi chetu Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kushiriki kwenye Tanzania the Royal Tour ambayo sasa hivi imetuwezesha unaona wawekezaji wanaendelea kuongezeka, unaona watalii wanaendelea kumiminika na mchango wa utalii kwenye Pato la Taifa, umeongezeka. Tukumbuke kwamba kwa mwaka 2014 mchango wa utalii katika Pato la Taifa ilikuwa ni asilimia 4.4 tu, lakini kwa mwaka jana 2022 ulipaa mpaka umefikia asilimia 17.5. Watalii wameongezeka kutoka 1,700,000 mwaka 2021 mwaka 2022 wamefika 3,800,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema ahsante sana Mama Samia Suluhu Hassan, tunasema ahsante sana kwa mikakati mliyoweka Wizara imeanza kuzaa matunda. Ombi langu kwenu ni kwamba watalii wamekuja ndiyo sasa lazima tuweke tuhakikishe kwamba huduma wanazozipata wakiwa ndani ya Tanzania kwenye mahoteli, kwenye ndege, kwenye mbuga ni za kiwango cha hali ya juu, kusudi kesho na kesho kutwa watamani kurudi ndani aya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera tunawashukuru sana, mwaka 2018 mlipandisha yaliyokuwa mapori ya akiba yakawa Hifadhi za Taifa tukapata Burigi - Chato, tukapata Ibanda, tukapata na Rumanyika, lakini kasi ya kuziendeleza hizo hifadhi ni ndogo sana. Tulitegemea kwamba baada ya kuzipata uongozi wa Mkoa wa Kagera walihakikisha kwamba wamefanya operesheni mbalimbali, wakaondoa mifugo yote iliyokuwa kwenye hifadhi hizo na mifugo mingine ilikuwa inatoka nchi za nje, uoto ukaongezeka wa asili, Wanyama wakaanza kurudi wanyamapori lakini na Serikali mkatusaidia kutuongezea wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunacholalamikia ni kwamba hatuoni kama kuna kasi ya kuziendeleza hizo hifadhi, kwa maana ya kutujengea barabara, njia zile routes, kuweka mahoteli, tunaona kwamba bado. Unakuta sehemu nyingi ndani ya hifadhi hizo hakuna mitandao. Sasa mtu ameenda kutalii amefika kule labda kapata shida akitaka kuwasiliana na mtu ambaye yuko nje ya hifadhi hawezi kwa sababu hakuna mtandao, au vijana wenyewe siku hizi wanataka wajipige picha karibu na mnyama, arushe ile picha na yule mtu aliye nje ya hifadhi aone hawezi kufanya hivyo kwa sababu hakuna mitandao. Tunaomba TANAPA itekeleze mpango mkakati wa kuendeleza hizo hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tupatiwe wataalam, kwa Mkoa wa Kagera tangu kwenye Mkoa mpaka ngazi zote za Halmashauri zote hatuna Afisa yeyote anayehusika na utalii. Kwa hiyo, utakuta mara ni Afisa Utamaduni, mara ni Afisa wa Misitu ndiye anapewa lile jukumu, yaani hatuna yule ambaye anaweza kwenda kwenye Halmashauri akatetea hata haki I mean ule mpango wa kuendeleza utalii. Kwa hiyo, tunaomba tupewe hao kusudi tuweze kuendeleza utalii Mkoani Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti ya mwaka jana Serikali mlituahidi kwamba sasa mnaenda kuchonga barabara kwenye hii Hifadhi ya Burigi - Chato lakini mkasema mnaenda kuanzisha utalii wa faru weupe kwenye hii Hifadhi ya Burigi - Chato. Naomba kujua kwenye bajeti hii kuna nini au kitu gani kimeshafanyika kwenye kuanzisha huo utalii wa faru weupe katika Hifadhi ya Burigi – Chato? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiomba kama mkoa lakini na Mheshimiwa Mbunge wa Biharamulo Eng. Ezra Chiwelesa amekuwa akiliongelea sana kwamba sasa lile lango la kuingilia Burigi - Chato lipite mahali ambapo wale wataliii sasa watatakiwa wapite katikati ya Biharamulo wakati wanaenda kwenye kutalii huko Burigi - Chato. Kusudi waweze kuchochea uchumi ndani ya Biharamulo Mjini, naomba kujua huo mpango umefikia wapi na nikuombe Mheshimiwa Waziri ukija kuhitimisha uniambie kwneye bajeti hii tulishapata hifadhi mpya zaidi ya moja Burigi - Chato ndiyo kuna mipango naiona kwenye bajeti, Je, hii Ibanda ya Kyerwa na Rumanyika ya Karagwe kuna mipango gani sasa ya kuziendeleza hizo hifadhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la tembo. Tembo wamekuwa tembo. Tembo tunawapenda, tembo ni maliasili tulipewa na Mwenyezi Mungu lakini sasa hivi wameamua kuhama kutoka kwenye hifadhi wanakuja mahali wanapoishi binadamu. Ukienda kule Missenyi kule Mabale, ukienda Karagwe kule Muramba ukaenda Kyerwa, ukaenda Ngara wanaingia kwenye mashamba, wanakula ndizi, haishii hapo hata na mgomba wenyewe anaula na anauchanachana unakuwa kama nyuzi. Wanaingia Kagera Sugar waanakula miwa ya Kagera Sugar, imekuwa ni kero, tunaomba msaada wenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna nyani na ngedere. Sisi huko Uhayani huwa tunalima mahindi yanawekwa kwenye mashamba ya migomba, sasa hawavuni maana yake ni ngedere na nyani ndiyo wanakuja kuvuna. Hata ukienda pale Manispaa ya Bukoba unakuta ngedere na nyani wanatambaa hata kwenye miji, kwa sababu huku zamani kila Halmashauri ilikuwa na kitengo kinaitwa bail in control, ambapo kulikuwa na Maafisa ambao walikuwa nahusika kuwavuna, kuwaua na kuwapunguza na kuwarudisha hifadhini wale wanyamapori wakali na wale ambao ni wasumbufu wanaharibu mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi hicho kitengo hakipo ndiyo maana hawa wanyama wanatawala na hakuna anayewashughulikia, tunawaomba mtuletee wataalam ambao wamesomea mambo ya wanyamapori ambao wanajua sasa ni kwa namna gani wanaweza kuwarudisha huko wanakotoka kusudi tusiendelee kuathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumebahatika na Mwenyezi Mungu akatupa vivutio vingi vya utalii. Nina uhakika kwamba kila Mkoa, kila Wilaya ikiwemo na Kagera kuna vivutio vingi, kwa sababu ya muda leo nitazungumzia vivutio vitatu tu. Mkoa wa Kagera tuna visiwa 48 ndani ya Ziwa Victoria ambavyo viko Mkoa wa Kagera. Kati ya hivyo 48 ni 27 vina watu wanaishi visiwa 21 hakuna mtu anayeishi pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ni opportunity ya kuweza kuanzisha utalii. Wizara tuende mkajenge mahoteli kule tuweze kuanzisha picnic sites, tuweze kuanzisha uvuaji wa Samaki - sports fishing, tuweze kuwa na utalii wa boti, mtu anasafiri kwenye boti anaendesha mwenyewe mtumbwi, anaenda upande ule kwenye kisiwa anastarehe na kurudi. Kwa hiyo, tunaomba tufanyiwe hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunayo misitu mikubwa, tunao msitu mmoja mkubwa unaitwa Minziro, huu msitu ni mkubwa una hekta zaidi ya 25,000 na inasadikiwa kulikuwa na nyoka mkubwa sana ambaye anaishi zaidi ya miaka 209 na huyo nyoka aliweza kuishi kwa siku zaidi ya 68 bila kula chakula anakunywa labda maji tu na katika msitu huo huo, nina uhakika watu wangependa kuja kuona msitu huo unafananaje. Lakini katika msitu huo huo kuna species nyingi aina ya miti mingi mamia na mamia na kati ya hayo mamia aina 12 ya miti hiyo inapatikana Tanzania tu, kwa hiyo nina uhakika watu wengi wangependa kuja kufanya utafiti na kuiona hiyo miti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao vipepeo wa rangi zote, tuna aina zaidi ya 600. Wanene, wembamba, wekundu, weusi, rangi zote wanapendeza ni kivutio tosha. Tunao ndege zaidi ya specie 238 na kati ya hao hizo specie 51 zinapatikana Mkoa wa Kagera tu. Huu msitu ukiendelezwa unaweza ukatuvutia utalii na watu wengi wakaja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mtufungulie utalii wa fukwe, Mkoa wa Kagera kwenye Ziwa Victoria tunayo fukwe moja nzuri sana ndefu. Ukianzia kule Muleba Kusini, ukaja Kaskazini ukaenda Kusini Kaskazini ukaja Bukoba Vijijini, Manispaa ya Bukoba ukaenda mpaka Missenyi ni fukwe moja ndefu sana ina mchanga mweupe mzuri na mawe mazuri ya ajabu. Mkiweza kuuendeleza ule ufukwe unaweza vilevile ukatuvutia utalii ambao utachochea kipato cha ndani ya Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Kwanza kabisa nampongeza Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mwigulu, Naibu Waziri Mheshimiwa Chande, Makatibu Wakuu kwa bajeti nzuri, bajeti kubwa ya shilingi trilioni 44.38 ambayo ina wagusa Watanzania wote, inaleta matumaini mapya. Kwa kweli Mheshimiwa Mwigulu na Mheshimiwa Chande mnafanyakazi nzuri sana ya kumshauri Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mambo makubwa na mazuri ambayo yanayoendelea kufanyika ndani ya Tanzania. Tunaona kwamba uchumi unaendelea kukua na kwa kutambua kwamba Watanzania wengi ni wakulima tumeona kwa jinsi gani bajeti ya kilimo ambavyo imekuwa ikipanda kila mwaka, lakini vilevile imekuwa ni tatizo na watu wengi wamelizungumzia. Sasa hivi Serikali imekubali inaenda kutoa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma kwenye vyuo vya kati, hawa ndio wataalamu tutakaohitaji katika viwanda vyetu, lakini hawa watoto au wanafunzi watapata stadi zitakazowawezesha waweze kujiajiri na hivyo tutakuwa tumepunguza tatizo la ajira katika Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali ya CCM kwa kuwajali watu wenye ulemavu kwa sababu nimeangalia kwenye bajeti hii ukurasa wa 10 unasema Serikali inaenda kutenga shilingi bilioni moja, iwekwe kwenye mfuko wa watu wenye ulemavu ili waweze kuweza kupata vile vifaa wanavyohitaji, Mheshimiwa Waziri bajeti ni nzuri hongereni sana kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda leo nitaongelea kitu kimoja tu; na nitaongelea Mkoa wa Kagera na umaskini ndani ya Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera ni maskini, lakini kwa fursa zilizo Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Kagera haupaswi kuwa maskini, Mkoa wa Kagera una ukubwa wa kilometa za mraba 35,686, una idadi ya watu wanakaribia milioni tatu, una mvua misimu miwili kwa mwaka, una wasomi kibao, umepakana na nchi jirani nne, lakini mkoa bado ni maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa za mwaka 2022 pato la mwananchi mmoja mmoja kwa kigezo hicho Mkoa wa Kagera ni mkoa wa mwisho katika Tanzania Bara kwa umaskini, lakini kwa miaka zaidi ya mitano consecutively Mkoa wa Kagera umekuwa kati ya mikoa mitano ya mwisho kichumi. Kwa hiyo, Mkoa wa Kagera ni mkoa maskini. Kwa kutumia kipimo cha umaskini wa mahitaji ya msingi (basic needs poverty), Mkoa wa Kagera una wastani wa asilimia 31.9 wakati wastani wa kitaifa ni asilimia 26.4 kwa maana hiyo Mkoa wa Kagera bado una hali mbaya kimaskini. Kwa kutumia kipimo cha umaskini wa chakula ambayo ni food poverty Mkoa wa Kagera una asilimia 12 wakati wastani wa Taifa ni asilimia nane. Kwa hiyo, inaonesha kwamba mkoa bado ni maskini zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera kama nilivyotangulia kusema kwa zaidi ya miaka mitano sasa unaendelea kuwa kati ya mikoa ya mwisho mitano kwa umaskini. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Waziri Mkuu statistics au takwimu huwa hazidanganyi, hivyo Mkoa wa Kagera tukubali, Mkoa wa Kagera una hali mbaya, umaskini umekithiri, lakini Wabunge tumeongea sana humu, kila Mbunge wa Kagera alipoinuka alizungumza juu ya umaskini wa Mkoa wa Kagera, mimi mwenyewe nafikiri ni mara ya tatu. Ukisoma kwenye mitandao ambayo imeundwa kwa watu wa Kagera wanaokaa Tanzania na wanaokaa nje kila mtu anaguswa na kila mtu anazungumzia juu ya umaskini wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile hata Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alipokuja mkoani Kagera kitu cha kwanza ambacho wazee wa Mkoa wa Kagera walimkabdidhi ni kwamba tunafanyaje, tunatokaje kwenye huu mkwamo ambapo kwa sasa hivi inaonekana kwamba mkoa wetu ni wa mwisho, ni mkoa maskini kuliko mikoa yote Tanzania Bara na yeye akatoa maagizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napenda Serikali mtueleze baada ya kuona mkoa ambao ulikua upo kati ya the best three, kati ya mikoa mitatu iliyokuwa inafanya vizuri kielimu, kati ya mikoa miatatu iliyokuwa inafanya vizuri kimaendeleo, sasa hivi umekuwa mkoa mwisho. Nina uhakika Mheshimiwa Mwigulu na wewe hili linakugusa, nina uhakikia Mheshimiwa Chande na wewe linakugusa na Waziri Mkuu na wewe na wote. Tunafanyaje? Mmeshafanya utafiti mkaleta REPOA, mkaleta kamati zenu hizo zinazoshauri kiuchumi katika Wizara wakaangalia tatizo ni nini ndani ya Mkoa wa Kagera? Kwa nini tunakuwa wa mwisho? Mnapopeleka hizi pesa mafungu yote miradi mnaleta, it doesn’t work bado tunaendelea kuwa wa mwisho. Kwa hiyo ina maana kwamba tunahitaji mkakati zaidi ya hizi hela za kawaida zinazopelekwa katika Mkoa wa Kagera na kwa sababu sasa sina muda nitaongelea mambo machache tu ambayo mimi nafikiri yakifanyika yanaweza kusaidia kufungua Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza biashara ya mpakani; sisi tunapakana na Uganda, tunapakana na Kenya, tunapakana na Rwanda, tunapakana na Burundi. Kwa kufanyabiashara tu ya mpakani ambapo ni eneo ninalofikiri Mheshimiwa Waziri wa Fedha naona kama Tanzania hatufanya vizuri kwenye kutafuta biashara ya kuendeleza biashara mipakani, lakini sisi kama Mkoa wa Kagera tunaona kwamba biashara ya mpakani ikiweza kuboreshwa inaweza ikatusaidia na kututoa katika mkwamo tuliopo.

Kwanza kabisa tunaomba tujengewe masoko, tujengewe soko pale Mtukula ambapo ni Misenyi kwenye mpaka wa Mrongo ambapo ni Kyerwa, kwenye mpaka wa Rusumo na Kabanga ambapo ni Ngara. Kwa kufanya hivyo tutafanya biashara na nchi jirani, na hii itafungua mkoa na kutakuwa na mzunguko wa pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifika sasa unaona kwamba hata wafanyabiashara wa Tanzania wanahama wanaenda kufanyiabiashara zao upande wa pili kwenye nchi jirani badala ya kufanyia Tanzania. Ni kwa sababu sera za kule, uharaka wa kuanzisha biashara kule, sera zao za kodi zinawavutia kuliko za hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali tujiangalie upya, tuangalie sera zetu mipakani zinasemaje kusudi tuweze kuwavutia sasa wasiende upande wa pili. Serikali ya Tanzania, National Housing imejenga mall pale Mtukula, lakini ni kwa muda mrefu imeshindwa kujaa, wafanyabiashara wana-prefer kwenda upande wa Uganda kuliko kufanyia Tanzania. Mlituahidi kutujengea pale soko, lakini ukienda ni vumbi tupu, wakati wa mvua ni matope matupu. Nani atakuja kuwekeza? Hakuna hata storage facilities. Tunaomba tujengewe masoko ya uhakikia kuweza kuufungua Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, lakini Mkoa wa Kagera mnajuwa tupo pembezoni ni mbali sana na Dar es Salaam ambapo ndio malighafi nyingi zinapatikana kilometa zaidi ya 1,500. Kwa hiyo, huyu mwekezaji ambaye anaamua kuwekeza ndani ya Kagera, cement wakati Dar es Salaam inanunuliwa shilingi 13,000; shilingi 15000 ikija kufika Kagera imekuwa ya shilingi 23,000 na shilingi 25,000. Gharama za uzalishaji zinakuwa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali mmeshajiuliza wakati mnahamasisha viwanda vingi vianzishwe watu wawekeze kwenye viwanda, kwa nini Mkoa wa Kagera tulipata wawekezaji wachache sana? Ni kwa sababu ya gharama za uzalishaji tuko nazo mbali sana, ndio maana mwaka 2015 Mkoa wa Kagera ulikuwa na kongomano la uwekezaji, waliomba na wameleta Serikalini na hamjatujibu, tunaomba tupate upendeleo maalamu (preferential treatment) ya kikodi, ya kisera, ya kisheria ili kusudi tuweze ku- compete, tuweze kuwa na ushindani kuwa na ushindani ulio sawa na nchi zilizo jirani ambapo inaonekana sera zao zinavutia zaidi, lakini mpaka leo hamjatujibu na sisi tunaendelea kuwa maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali mtusaidie kwa kuboresha biashara za mipakani, lakini vilevile tupate hiyo preferential treatment ili tuweze kushindana na kuboresha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera ni predominantly rural yaani maeneo mengi yamekaa kama vijiji. Kwa hiyo, kitu cha kututoa sasa ni kilimo, Mheshimiwa Bashe kitu cha kututoa kwenye umaskini Mkoa wa Kagera ni kilimo. Tunalima kilimo ambacho hakina tija, matumizi ya mbolea yako chini sana, mazao/mimea tuliyokuwa nayo ni imezeeka, kwa hiyo tunaomba Serikali waje watusaidie watupe pesa kusudi tulime kilimo ambacho kina tija, wang’oe ile mibuni na migomba ya zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara ya kwanza mwaka jana Serikali ndio imetuletea mbolea tani 2,600 yenye thamani ya shilingi bilioni 7.5 na kati ya hizo shilingi bilioni nne zote zilikuwa ni ruzuku iliyotolewa na Serikali, tunasema ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri awahamasishe Wanakagera walime kwa kutumia mbolea ili tuweze kupata kilimo chenye tija, lakini vilevile tunapopata ushuru haya mazao yote yakiuzwa kahawa ikiuzwa, kwa mfano kama mwaka jana ushuru kutoka kwenye kahawa ilikuwa shilingi bilioni 4.5, ni kiasi gani kilirudishwa katika kuendeleza zao la kahawa? Unakuta kwa sababu Halmashauri zina mambo mengi yanayofanywa haziwezi kuendelea kurudisha hela kwenye kilimo zinaenda kwenye huduma kama afya, kama maji ni vizuri, lakini ni kiasi gani kinachorudi kuendeleza kilimo? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba Wizara ya Kilimo…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba yako mengi ya kuongea Waziri wa Fedha anapokuja kuhitimisha tunaomba atueleze kuna mpango gani makusudi wa kuweza kwenda kusaidia Mkoa wa Kagera, kuutoa kwenye mkwamo, waondoke kuwa mkoa wa mwisho wa umaskini ndani ya Tanzania, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti hii. Kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Ummy Mwalimu; Naibu Waziri, Dkt. Faustine Ndugulile; Katibu Mkuu, Dkt. Mpoki kwa hotuba nzuri ya bajeti, lakini vile vile kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii na katika sekta ya afya, kwa kweli nafasi walizopewa wanazitendea haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuonesha nia ya dhati ya kuiendeleza na kuiboresha sekta ya afya lakini pamoja na kazi zingine nzuri anazoendelea kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kupongeza kwa sababu kuna mambo makubwa yamefanyika katika Wizara hii. Kwanza, tumesikia hapa wanavyotuambia kwamba sasa hivi wanatoa chanjo dhidi ya kirusi cha papilloma (papillomavirus) ambacho kinasababisha saratani ya shingo ya kizazi kwa wasichana wa miaka 14. Hiki kitu kilikuwa hakijawahi kutokea Tanzania hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nakumbuka mwaka jana kulikuwa na makelele mengi na hasa mwaka juzi, juu ya kwamba hakuna dawa. Sasa hivi upatikanaji wa dawa umepanda mpaka asilimia 80 hadi asilimia 90, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa kusambaza ambulance nyingi katika vituo vingi kuliko miaka mingine yoyote ile. Nipende kuwapongeza sana Muhimbili, nampongeza Mkurugenzi wa Muhimbili, Dkt. Maseru kwa kazi nzuri ameirudisha Muhimbili kwenye chart, watu walikuwa wameshaikimbia, sasa hivi huduma zimekuwa nzuri kila mtu anataka kuja kutibiwa Muhimbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza watu wa MOI, Mkurugenzi wa MOI pamoja na watalaam wake wote. Sasa hivi wanafanya operation za magoti, za nyonga, lakini vile vile wameweza kufanya operation ya mgongo kwa njia ya matundu (laparoscopy) kwa mara ya kwanza ndani ya Tanzania, hongereni sana kumbe wataalam wetu wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumpongeza Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo, Profesa Janabi kwa kazi kubwa sana ambayo anaifanya. Tunakumbuka watoto wengi walikuwa wanapelekwa nje ili kuzibwa matundu yaliyo kwenye moyo, wao wanafanya sasa hivi. Betri maalum pacemaker zinawekwa kwenye moyo. Wameweza kufanya upasuaji wa mishipa kwa kutumia lazer, nilikuwa naisoma kwenye vitabu kumbe sasa hivi inafanyika Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile wameweza kufanya upasuaji wa moyo wakapandikiza mishipa bila kusimamisha moyo, kwa kweli wanastahili heko, hongereni sana. Mwisho wameweza kupandikiza hata na figo, kwa kufanya hivyo wameokoa pesa nyingi za kitanzania ambazo tungeweza kutumia kwa kwenda kutibiwa nje. Nipende kumkumbusha Mheshimiwa Waziri, kwamba watu wanaofanya vizuri namna hii haiwezekani bajeti yao ikapungua; sasa naomba waongezewe bajeti, waongezewe fedha, kusudi waweze kufanya makubwa zaidi ya hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mazuri yanayofanyika lakini bado kuna upungufu mkubwa wa watumishi na nafikiri huu umesababishwa kwa sababu utoaji wa huduma za afya umepanuka. Tumeongezea vituo vya afya, tumeongeza zahanati, tumeongeza hospitali, obviously lazima watumishi wapungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa kwa kuwa kuna upungufu ni kilio cha kila mtu Serikali waliangalie kwa jicho la zaidi, kwa sababu hata kwenye hospitali tunazoziita hospitali maalum kama ya Benjamin Mkapa ambayo ina vifaa vingi vizuri vya kila aina lakini bado kuna upungufu wa watumishi. Ukienda kwenye hospitali za Kanda kama Bugando nayo unakuta kuna upungufu wa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Bugando ni Hospitali ya Rufaa kwa Kanda ya Ziwa. Mikoa yoyote ya kanda ya ziwa tunategemea Bugando. Tunawashukuru kwa kutuletea hata kituo cha kansa pale. Hata hivyo ukienda hasa upande wa chemotherapy unakuta kwamba hakuna wataalam. Tunaomba aidha wawapelekee wataalam wa kutosha au wale waliopo basi waweze kuwa-train kusudi watu wanaotoka Kanda ya Ziwa waweze kupata huduma za afya zilizoboreka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Mkoa wa Kagera kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya. Kati ya watumishi 6,245 wanaohitajika tuna 2,575 tu; kwa kweli ni upungufu mkubwa sana. Hata ukiangalia kitaifa upungufu wa watumishi ni asilimia 48; hii ni hatari kwa sababu pamoja na kupeleka dawa; tunasema dawa ziko kule kwa asilimia mpaka 90 kama hakuna daktari wa kuandika, hakuna muuguzi wa kuitoa hiyo dawa, kwa hiyo ina maana kwamba tutakuwa tumefanya kazi bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tusije tukaharibu kazi nzuri tunayofanya basi naomba, kwa kuwa tunajua wapo Madaktari wengi mitaani ambao tayari wako trained lakini hawajaajiriwa na kwa kuwa juzi Mheshimiwa Mkuchika ametutangazia kwamba sasa kuna mafuriko ya ajira. Ajira zaidi ya elfu arobaini zitatolewa, tunaomba vibali vitolewe vingi kwa ajili ya sekta ya afya ili watu wetu waweze kunanii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile niwaombe waendelee kuwa-train wale Madaktari Bingwa ili waweze kutoa tabibu za kibingwa katika hospitali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera uko pembezoni…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Bukoba ina Wataalam watatu tu, wa meno, akinamama na mama wajawazito. Hata hivyo, kama mtu ni mahututi lazima akimbizwe kwenda mpaka Bugando Mwanza. Anatumia masaa nane mpaka 10 wakati ambulance waliyokuwa nayo ni mbovu, spare hamna. Mheshimiwa Ummy nimeshampelekea hilo tatizo, Mheshimiwa Waziri Mkuu nilishamwambia, naomba kujua je, katika hii bajeti wataweza kutupatia hii ambulance kusudi tuweze kuondoa hizo kero. (Makofi/vicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera unahitaji hospitali nane za wilaya lakini tunazo mbili tu, kwa hiyo tulikuwa tunaomba, kwa sababu sasa hivi kila mtu anataka kwenda kutibiwa kwenye Hospitali ya Serikali.; tunaomba sasa tupatiwe Hospitali ya Serikali ya Wilaya ya Biharamulo, Hospitali ya Bukoba Vijijini, Hospitali ya Karagwe, Hospitali ya Wilaya ya Kyerwa, Hospitali ya Wilaya ya Missenyi na Hospitali ya Wilaya ya Muleba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutoa hela za kukarabati vituo ambapo walikuwa wanatoa kati ya milioni mia nne mpaka mia tano. Kwa bahati mbaya Manispaa ya Bukoba hawajapata fedha hizo. Tunaomba na Manispaa ya Bukoba waweze kupatiwa hizo fedha milioni mia nne mpaka mia tano ili waweze kukarabati hivyo vituo vya afya na hii itawasaidia kutoa huduma bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni bima ya afya. Bima ya afya ni muhimu sana ndugu zangu. Matibabu ni gharama mpende msipende, kuna siku utaugua huna hata senti tano ndani ya nyumba, lakini unaweza kwenda hospitali wakakwambia vipimo vinaenda mpaka laki nne mpaka laki tano. Unaweza ukaambiwa kuna operation ambapo inaenda mpaka milioni, huna hata senti tano utafanyaje. Kama tungekuwa kwenye mfumo wa bima ina maana tunabebana mchango wako, mchango wa huyu unampeleka yule na wewe ikiwa zamu yako unapelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia watu walio kwenye mfumo wa bima ya afya sasa hivi ni asilimia 32 tu, kwa hiyo napendekeza kwamba sasa Wizara ya Afya mfanye mtakachoweza kufanya, mfanye uhamasishaji mkubwa huko vijijini watu wengi waweze kujua umuhimu wa bima ya afya kama walivyosema kwamba wanaleta universal health coverage; kusudi kila mtu aweze kuingia kwenye mfumo wa afya na tuweze kutoa afya bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naendelea kuwapongeza kwa kazi nzuri wanayo… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BERNADETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa na mimi nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wakuu katika Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa mpango wake wa elimu bila malipo. Serikali imetoa hela nyingi, inatoa zaidi ya shilingi bilioni 23.8 kila mwezi kugharimia elimu lakini katika waraka uliotoka na wazazi walipewa majukumu fulani, wazazi walibakiwa na jukumu la kuhakikisha kwamba wanatoa uniform pamoja na chakula kwa ajili ya watoto wao. Wasiwasi wangu ni maelekezo yaliyotoka Wizarani au tuseme TAMISEMI kwamba hiki chakula ili mwanafunzi aweze kukila shuleni utaratibu utakuwa tofauti na ule uliokuwa unatumika kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua umuhimu wa chakula au umuhimu wa lishe. Mtoto akiwa na njaa hawezi kujifunza na akaelewa. Tunatambua kwamba Watanzania chakula cha jioni tunakula kati ya saa 11.00 jioni mpaka saa 2.00 usiku, mtoto tangu saa hizo hajapata kitu chochote, anaamka asubuhi hakuna breakfast anaenda shuleni anasoma tangu asubuhi mpaka jioni, hawezi kuelewa kitu chochote.

Naomba basi Wizara ya Elimu ile ya kusema kwamba chakula kikichangwa, michango ikichangwa, wazazi wenyewe waji-organise awepo mtu atakayeratibu kukusanya hivyo vyakula ndiyo viweze kupikwa mashuleni watoto wale, nafikiri si sahihi. Hili ni jukumu la msingi la walimu, kwa hiyo, jukumu la chakula kinaliwa na nani na saa ngapi waachiwe walimu lakini wazazi watimize jukumu lao la msingi la kuhakikisha kwamba watoto wao wanapata chakula mashuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa walimu mashuleni ni mkubwa sana kitaifa, lakini vilevile ukiangalia kwenye Mkoa wa Kagera ninakotoka kuna upungufu wa walimu zaidi ya 6,773 katika shule za msingi na katika shule za sekondari kuna upungufu mkubwa sana wa walimu wa sayansi na hisabati. Najua kila nchi ina mipango yake na ina namna ya kuandaa wataalam. Napendekeza kwa hili Serikali ingefanya mpango, tuna Chuo Kikuu cha Dodoma hapa, kina majengo yako pale, wangeweka mkakati sasa wa kwamba hicho chuo sasa hivi kitumike kuwaandaa walimu wa sayansi, hisabati pamoja na walimu wa shule za msingi ambao wanakosekana kusudi katika miaka miwili, miaka minne tuwe tumemaliza hili tatizo. Chuo cha Dodoma kipo na kinaweza kikafanya mpango huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zinaonesha kwamba kwenye shule za msingi namba ya watoto wa kiume na wa kike inalingana; ukienda sekondari namba ya watoto wa kike na wa kiume zinakaribiana na ukienda kwenye vyuo vikuu namba ya watoto wa kike inaendelea kupungua lakini kwenye masomo ya sayansi imepungua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko kwenye Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, wamegundua kwenye vyuo viwili kuna 17% tu ya wasichana wanaosoma masomo ya sayansi kwenye vyuo vikuu. Hii ni hatari, haiwezekani Tanzania tukasema kwamba tunaendelea wakati nusu ya Watanzania wanaachwa nyuma ambao ni wanawake. Pia tukumbuke kwamba hawa wasichana ambao mnawaona kwamba ni wachache sana katika masomo ya sayansi kwenye vyuo vikuu ni walewale watoto wa kike ambaye akitoka shuleni, akirudi nyumbani kwanza amsaidie mama kutengeneza chakula na kufanya usafi. Yule yule mtoto wa kike ikitokea mzazi au mlezi ni mgonjwa lazima abaki nyumbani kumsaidia. Hawa watoto wa kike akiwa shuleni anashawishiwa na watoto anaolingananao, anashawishiwa hata na mababa watu wazima, yote inamletea msongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, akiwa kwenye jamii au darasani kuna mtazamo kwamba masomo ya sayansi na hisabati ni kwa ajili ya wanaume, wasichana hawafai huko. Kwa hiyo, siku za nyuma tulikuwa na mpango kila walipokuwa wanamaliza form six wale watoto wote wa kike ambao walikuwa wanakaribiana na ufaulu ambao unatosha kumuingiza chuo kikuu walikuwa wanapelekwa chuo kikuu wiki sita kabla ya kufungua vyuo vikuu, wanapewa some kind of an induction course na baada ya hiyo course walikuwa wanapewa mtihani, wanashinda na wengi walifanya hivyo na wakashinda kuliko hata wale waliopata division one. Niiombe Serikali huu mpango urudishwe ili watoto wa kike wanaomaliza form six ambao ushindi wao ni mzuri kidogo yaani wameteremka kidogo kuliko ule unaohitajika wapelekwe chuko kikuu kusudi waweze kufanyiwa hiyo induction course. Hii itaweza kungeza wanafunzi katika vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera mnajua kwamba lilitokea tetemeko na shule nyingi ziliharibiwa, miundombinu iliharibiwa na watu walifariki. Niipongeze Serikali kwa kazi nzuri mliyoifanya pale Iyungo secondary school, mmeijenga imekuwa ya kileo ni maghorofa matupu. Hongereni sana na Nyakato inaendelea kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka kuwaambia kwamba bado kuna shule kama Bukoba secondary school na Rugambwa secondary school zote ni za Serikali, ni shule kongwe na ziliathiriwa na tetemeko. Nauliza Serikali ina mpango gani wa kuzikarabati shule hizi kwa sababu walimu na wanafunzi kwenye shule hizo wanaishi katika hali hatarishi kwa sababu kwanza yale majengo ni ya zamani, halafu yalitetemeka lakini sijaona mpango uliopo kwa ajili ya kuzitengeneza au kuzirekebisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufikia uchumi wa kati ambao utatawaliwa na viwanda na ili hii ndoto itimie lazima watoto wajifunze sayansi. Tuna upungufu mkubwa sana wa maabara. Mkoa wa Kagera tu tuna upungufu wa maabara 352 ambayo ni 62% ya mahitaji na hizi maabara zote zimejengwa kwa nguvu za wananchi. Napendekeza Serikali ingetenga hela maalum kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanajenga maabara kila shule za chemistry, physics, biology, geography na ikiwezekana computer lab ili tuweze kufikia kwenye huo uchumi wa viwanda ambao tunauzungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni vyuo vya VETA. Napongeza mpango wa Serikali wa kuendelea kujenga hivyo vyuo vya VETA. Uchumi wa viwanda utahitaji hawa mafundi wa katikati. Ni bahati mbaya sana mimi wakati nasoma na nafundisha tulikuwa hata na shule za ufundi lakini na zenyewe zimekufa. Napendekeza kwamba tuendelee na mpango huohuo ili katika kila…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu kwa kazi nzuri wanayoifanya kwenye sekta ya maji. Nawapongeza kwa sababu upatikanaji wa maji umeongezeka pamoja na kuwa bado yapo maeneo ambayo hawajapata maji safi.

Mheshimiwa Naibu Spika, inasikitisha kuona kuwa Serikali inaweka mikakati mikubwa ya kuongeza upatikanaji wa maji nchini, lakini maji mengi sana yanapotea sababu ya uchakavu wa miundombinu. Hili ni tatizo kubwa, inafifisha kazi nzuri inayofanywa kwenye sekta ya maji. Je, katika bajeti hii zimetengwa fedha za kutosha kuboresha au kukarabati miundombinu ya maji iliyochakaa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko Taasisi na Idara za Serikali ambazo wanatumia maji, lakini hawalipi ankara za maji, inabidi kila mtumiaji wa maji alipe maji kama Mheshimiwa Rais alivyoagiza. Kama hawalipi wakatiwe huduma. Na mimi naona wakatiwe ili walipe kusudi kuzipa nguvu Mamlaka za Maji ziweze kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa mpango wao wa kuiweka Bukoba Mjini kwenye mpango wa kuandaa mfumo wa kuondoa maji taka. Tatizo hili limekuwa la muda mrefu. Taka hizi hutiririsha maji machafu kwenye mfereji hadi ziwani. Nawapongeza French Development Agency- AFD. Je, mradi huu utaanza lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji Wakuu kwa kazi nzuri inayofanyika katika Wizara ya Viwanda na Biashara. Wengi hawakuamini kuwa Tanzania ya viwanda inawezekana hayawi, hayawi, sasa yamekuwa. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa viwanda vingi ambavyo vimeanzishwa nchini, viwanda hivi ndivyo vitaipeleka nchi yetu kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamehamasika kuanzisha viwanda, wanachohitaji ni kuwa karibu nao ili wapate ushauri wa kina. Wanahitaji ushauri/elimu juu ya aina ya viwanda vinavyofaa kuanzishwa katika maeneo yao, viwanda vitakavyotumia malighafi zinazopatikana karibu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa wanahitaji ushauri wa kitaalam wa hatua za kufuata katika kuanzisha kiwanda (usajili, tozo, kodi, uthibiti na kadhalika) watu hawa wangependa kupata ushauri wa kitaalam wa namna ya kupata masoko. Wanahitaji kujua wapi mitaji rahisi inapatikana. Mheshimiwa Waziri aliwahi kusema kuwa upo mwongozo wa namna ya kuanzisha viwanda, tunaomba huo mwongozo usambazwe na wengi wausome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa mingi imeanza kupiga hatua kwa sababu wapo wafanyabiashara wengi wamewekeza kwenye Mikoa hiyo. Mkoa wa Kagera utaendelea kubaki nyuma sababu uwekezaji Mkoani wa Kagera uko chini sana, chini ya asilimia mbili. Wawekezaji wengi wanauona kuwa Mkoa wa Kagera uko pembezoni, uko mbali na kadhalika. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha wawekezaji ili wakubali kuja wengi kuwekeza Mkoani Kagera?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri kwa kazi nzuri mnayoifanya kwenye kilimo na ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni muhimu sana katika kuleta maendeleo ya Mtanzania. Huwezi kuleta maendeleo ya Tanzania kama wakulima ambao ni asilimia 70 watakuwa wamekosa kuendelezwa/wameachwa nyuma. Kwa sasa kilimo kinacholimwa hakina tija, bado wanatumia zana duni kama jembe la mkono, hawalimi kitalaam, wanalima kilimo cha kujikimu siyo kilimo cha biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji tuwe na Maafisa Ugani ili waweze kuwaelimisha/kushauri wakulima.Kuna upungufu mkubwa sana wa maafisa ugani. Mkoa wa Kagera tuna upungufu wa Maafisa Ugani takribani 500 lakini wako ngazi ya kata. Kata moja ina vijiji vitatu mpaka sita, hana vitendea kazi hana hata pikipiki, atawazungukia vipi wakulima? Napendekeza waajiriwe Maafisa Ugani kwenye ngazi ya kila kijiji. Hawa wakitosheleza wakafanya kazi yao ya ugani, tutainua kilimo, tutapata malighafi ya viwanda katika uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya kahawa ni mbaya sana, kilo moja inauzwa kwa shilingi 1,000. Mbuni ukiupanda utatumia miaka miwili mpaka mitatu kuanza kuzaa kahawa. Zikianza kuzaa unaulea mbuni kwa mwaka mzima ukipalilia, ukiweka mbolea, unapulizia dawa unaishia kupata shilingi 1,000 tu kwa kilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu mkulima wa kahawa ameendelea kuwa maskini kwa sababu ya bei ndogo ya kahawa. Amekata tamaa ya kuendelea kulima kahawa. Serikali imependekeza kuondoa tozo 21 zifutwe. Nawaunga mkono hoja kwa hili lakini ili haya yasibakie kwenye makaratasi tu, baada ya bajeti hii. Wawakilishi wa wananchi (Wabunge) kutoka maeneo yanayolima kahawa tukutane na watalaam, tupitie mpango mkakati wa kupandisha bei ya kahawa kiukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndizi kwa mtu wa Kagera ni zao la chakula, ni zao la biashara ya migomba imeshambuliwa na ugonjwa mbaya wa mnyauko, ni janga. Wakulima wanashauriwa mgomba ukigundulika una mnyauko, anaambiwa kata/ng’oa/zika. Matokeo yake mashamba yamebaki yakiwa wazi/matupu.Migomba imeisha sababu ya kung’olewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo miche ya migomba isiyoshambuliwa na mnyauko. Kwa kiasi kikubwa wanategemea maabara ya Arusha ni mbali sana na Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kagera kuna Kituo cha Utafiti cha Maruku ambao wanao watalaam lakini hawana maabara kubwa, wanategemea Arusha. Naomba ili kumsaidia mkulima wa Kagera kumuondolea umaskini zitolewe fedha nyingi za kutosha, ili Kituo cha Utafiti cha Maruku waweke maabara kubwa. Wazalishe tissue, culture. Miche safi isiyo na vimelea vya mnyauko isambazwe kwa wakulima wengi waondokane na gonjwa baya la mnyauko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu kwa hotuba nzuri na kazi nzuri inayofanyika katika Wizara.

Mheshimiwa Spika, niongelee kuhusu Ranchi za Taifa. Kumekuwa na malalamiko makubwa ya siku nyingi kuhusu wananchi wanaoishi karibu na Ranchi za Taifa maeneo yaliyogawanywa katika blocks (vitalu) kukosa malisho. Wananchi wanaoishi Misenyi katika Kata ya Kakunyu, Kijiji cha Bubale na vijiji vingine katika kata hiyo maeneo yao yalitwaliwa, watu wakagawiwa blocks na wananchi wazawa/wakazi wakakosa mahali pa kulima na kufugia. Wamesema, wamepiga kelele, wamepaza sauti lakini sauti zao hazisikiki.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amesema wale walioshindwa kuendeleza vitalu walivyopewa watanyang’anywa wapewe wawekezaji wengine wenye ng’ombe wengi. Nauliza swali, vipi sasa hawa wananchi wakulima/wafugaji ambao maeneo yao yalitwaliwa na hawana maeneo? Kwa kuwa kwenye vijiji hivi watu wameongezeka (population), naomba yatengwe maeneo zaidi na haya yarudishwe kwa wananchi wa kawaida ambao ni wakulima/wafugaji.

Mheshimiwa Spika, pili, hawa wafugaji wadogo wadogo wanahitaji kuendelezwa. Waliambiwa wajiunge kwenye vikundi vikundi watapewa maeneo ya kufugia. Napendekeza tusipendelee wawekezaji peke yao, itafutwe namna ya kuwaendeleza wafugaji wadogo wadogo pia kwa kuwapa maeneo ya kufugia, kuwapa elimu juu ya uboreshaji wa malisho na mifugo. Bajeti hii haioneshi ni kwa namna gani inapanga kumuendeleza mfugaji mnyonge.

Mheshimiwa Spika, sababu ya uvuvi uliopitiliza (over fishing), samaki wamepungua sana kwenye Ziwa Victoria. Ili kulipunguzia mzigo Ziwa Victoria, kuongeza samaki na kuwaletea mapato wananchi na hivyo kukuza uchumi ni vizuri wananchi wakaendelea kuhamasishana ili wafuge samaki.

Mkoa wa Kagera watu wengi wameitika/wamehamasika, wamechimba mabwawa na kufuga samaki, tatizo hao samaki hawanenepi hata baada ya miezi nane au kumi bado wanakuwa na uzito mdogo sana. Tatizo ni kuwa wakulima hawajui mbegu bora iko wapi, hakuna Maafisa Ugani wa kuwashauri wafugaji wa samaki na pia chakula sahihi ni shida. Je, ni lini Serikali itatenga pesa za kutosha na kuendeleza ufugaji wa samaki wa mabwawa?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji Wakuu kwa kazi kubwa ya kutunza amani nchini, Mheshimiwa Waziri hongera sana na ni ukweli usiopingika kwmba, kazi nzuri inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalipongeza Jeshi la Polisi hasa Dawati la Jinsia kwa kazi nzuri wanayofanya, limekuwa kimbilio la wanyonge na wenye manyanyaso mbalimbali. Dawati hili lilitoa takwimu juu ya ukatili majumbani, wanawake wanaoteswa, wanaopigwa, kubakwa na kuuawa zinatisha lakini takwimu za watoto wanaoteswa, wanaolawitiwa/kubakwa ni kubwa mno. Napenda kujua Wizara ina mpango gani ili kudhibiti ukatili mkubwa wanaofanyiwa wanawake na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku wanakamatwa wahamiaji haramu wanaoingia nchini kinyume na utaratibu. Hawa watu wanaweza kuingia na kuingiza silaha kitu kinachohatarisha usalama wa nchi yetu. Najua mipaka yetu iko porous, napenda kujua Jeshi la Polisi/Wizara wana mpango gani wa kudhibiti uingizaji wa silaha kupitia mipaka yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. BERNADETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri kwa kuwasilisha vizuri hotuba hii na kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuwa wasikivu. Waziri ametoa tamko Bungeni kuwa watumishi walioajiriwa kabla ya mwaka 2004, waliosimamishwa kazi sababu walikuwa na cheti cha darasa la saba hawana cha kidato cha nne warudishwe kazini. Nawapongeza Serikali kwa kuwarudisha kazini na kuwalipa mishahara yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo sasa ni wale walioajiriwa tangu mwaka 2004 na kuendelea wamesimamishwa, hawa hatma yao ni nini? Hawa ni watu wa hali za chini na kawaida, ni maskini, ni wanyonge, wametumikia nchi hii kwa zaidi ya miaka 10, je, Serikali itawasaidiaje kwa sababu hawa wa darasa la saba hawaajiriki tena. Fedha zao zilikatwa zikawekwa kwenye Mifuko ya Hifadhi za Jamii mfano NSSF, uwezekano wa kuajiriwa haupo sababu ni darasa la saba. Naomba ili kuwasaidia warudishiwe michango yao iliyo kwenye hii mifuko, Serikali inasemaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu. Naanza kwa kumpa pongezi Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote Wakuu kwa kuandaa bajeti nzuri. Kwa kweli, bajeti hii ni nzuri, nasema ni nzuri kwa sababu bajeti hii imewalenga watu wa kawaida na ukiangalia mipango iliyopo unaona kabisa kwamba, bajeti yetu hii inawalenga watu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia bajeti hii imelenga kupunguza matumizi na gharama za maisha, lakini imelenga kuhusianisha ukuaji wa uchumi pamoja na maendeleo ya mtu mmoja mmoja. Bajeti hii imelenga kuendeleza viwanda na wakishaendeleza viwanda ina maana kwamba, wakulima watatoa hizo malighafi, watapata mahali pa kuuza bidhaa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema bajeti hii ni nzuri kwa sababu unakuta kwamba, inalinda viwanda vyetu vya ndani. Sasa hivi tunasema tuko katika era ya kukuza viwanda katika Tanzania kwa hiyo, lazima tuvilinde viwanda vyetu vya ndani, ndiyo maana nimefurahishwa niliupoona kwamba, katika bajeti hii wanaondoa kodi ya ongezeko la thamani kwenye vifungashio vya dawa za binadamu, kwa hiyo mtu wa kawaida atapata dawa kwa bei nafuu. Vilevile virutubisho vya vyakula vya mifugo, kama vyakula vya kuku vinaondolewa VAT kwa hiyo, vitazalishwa kwa bei nafuu, mkulima atafuga na kuweza kupata faida kwa sababu gharama za uzalishaji zitakuwa ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile bidhaa zinazozalishwa humu nchini kama juice, bia, maji, mvinyo, vinywaji baridi, ushuru haukupanda kwa hiyo, gharama za uzalishaji zitakuwa ndogo, therefore wataweza kuzalisha kwa faida. Mheshimiwa Mpango hongera sana pamoja na Naibu Waziri kwa kutuletea bajeti nzuri ambyo inalenga watu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata ukiangalia kwenye Ibara ya 43 kwenye bajeti hii ambayo inazungumzia vipaumbele, kipaumbele cha kwanza kilichozungumzwa ni kilimo, kilimo ndiyo sekta ambayo inaajiri Watanzania walio wengi. Hongereni sana ni bajeti ya watu ni bajeti ambayo inawalenga Watanzania wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, watoto wa kike wanashindwa kwenda shule kati ya siku mbili mpaka nne kila mwezi kwa sababu ya maumbile. Kwa kipindi kirefu sana Wabunge Wanawake mnatuona huwa tunakwenda pale Pius Msekwa kwenye Ukumbi tunafanya mikutano mbalimbali, baadaye tukawaomba na wanaume wakatuunga mkono, tunapanga mipango, tukaunda Kamati mbalimbali zikaenda kuongea na Serikali, hatimaye Serikali ya Chama cha Mapinduzi imekubali ikaliona hili na kuondoa kodi ya VAT kwenye taulo za kike ili kusudi watoto wa kike waweze kuzipata kwa bei nafuu na wakishazipata kwa bei nafuu ina maana sasa hata wataweza kwenda shule kila siku kwa sababu wataweza kujisitiri, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kupanga kuleta mabadiliko ya Sheria ya Serikali za Mitaa ambayo inasema sasa asilimia 10 zitengwe, kwa ajili ya asilimia tano kwa wanawake na vijana asilimia tano. Pamoja na kwamba, viongozi mbalimbali hasa Mawaziri walikuwa wanakaa hapa wanatuambia hizo asilimia zitengwe, lakini Halmashauri nyingi walikuwa wanakwepa, hawatengi asilimia 10, wakitenga ni asilimia mbili au tatu. Sasa sheria ikishakuja itawabana itabidi wazitenge hizo asilimia.

Mheshimiwa Spika, nataka kuwaambia mimi najishughulisha sana na vikundi vya vijana na vikundi vya wanawake kwa kweli, hizi hela zinasaidia. Hizi hela zikienda kwenye vikundi vya vijana wataweza kufanya shughuli zao, watakuwa wamejiajiri, akinamama watafanya biashara zao, watafanya ujasiriamali, wataweza kulisha hizo familia.

Mheshimiwa Spika, leo hii naleta kero kubwa ya wakulima wa Mkoa wa Kagera na kero yenyewe ni bei ndogo sana ya kahawa. Unakuta mtu analima kahawa, anautunza mbuni kwa miaka miwili mpaka minne katika miaka hiyo analima, anapalilia, anaweka mbolea, anaweka viua- wadudu, lakini anakuja kuuza kilo moja ya kahawa kwa Sh.1,000. Hii ni bei ndogo sana, pamoja na kwamba Serikali ilitangaza kati ya tozo zile 26 zilizokuwa kwenye mazao mbalimbali zilipunguzwa, lakini bei ya kahawa haikupanda.

Mheshimiwa Spika, hata leo hii msimu wa kahawa umefunguliwa, lakini bei bado ni ndogo. Ni ndogo kwa sababu, hadi leo mtu akiuza kahawa kilo moja unakuta kuna ushuru wa Halmashauri ya Mji Sh.84, kuna ushuru wa Chama cha Msingi Sh.200, kuna ushuru wa Chama Kikuu, kuna ushuru wa sijui uboreshaji, usafirishaji, ukaushaji shilingi Sh.330, kuna gharama za mikopo, yaani wao wanakopa, riba wanaiweka kwenye kila kilo ya kahawa inayouzwa Sh. 367 na gharama nyingine zinakuja mpaka Sh.1,600.

Mheshimiwa Spika, unakuta mtu labda kahawa kwenye World Market imeuzwa kwenye Sh.3,000, lakini Sh.1,600 zote zinakatwa, lakini na mwenyewe akienda kuuza anapewa malipo ya awali labda kama Sh.1,000/=, wanasema wakishauza kule watakuja kumpa malipo ya pili na malipo ya pili na yenyewe huwa hawapati.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia kwenye kitabu kinachozungumzia hali ya uchumi hapa naona kwamba, uzalishaji wa kahawa umepungua kwa 20.7% wakati uzalishaji wa korosho umepanda kwa 70.7%. Hakuna muujiza hapa, muujiza ni bei, bei ya kahawa ikipanda watu wenyewe watalima, watakata ile mibuni ya zamani, watalima mipya. Tunaomba vituo vya utafiti kama TACRI wapewe fedha watengeneze miche bora, wasambaze kwa wakulima walime kwa tija waweze kuuza mazao kwa bei zinazoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeshangaa kwenye hiki kitabu cha hali ya uchumi wanazungumza kwamba, kwa mwaka 2017 kahawa ya robusta na arabika iliweza kuuzwa kati ya Sh.4,200 mpaka Sh.5,900 sasa inakuwaje mkulima anapata Sh.1,000 jamani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ndiye jembe letu na ndiye tegemeo letu. Tunaona amefanya kazi nzuri sana kwenye mazao mengine kama korosho, tumbaku na pamba. Wote hapa Wabunge wanaotoka kwenye mikoa inayolima kahawa tunaomba na kwetu aje atusaidie, bei ya kahawa ipande ili kusudi watu wa kwetu waweze kuondokana na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana waliyoifanya kwa kujenga upya shule ya Ihungo na Nyakato Secondary School ukaifanyia ukarabati wa kina baada ya kuwa shule hizi zimeharibiwa sana kwa tetemeko. Sasa hivi shule zimekamilika lakini hakuna samani, kwa sababu baada ya tetemeko wanafunzi walisambazwa kwenye shule mbalimbali katika Mkoa. Sasa zile samani walihama nazo na katika hamisha hamisha samani zikaharibika.

Mheshimiwa Spika, watoto wanapaswa kuingia form five mwezi wa Julai/Agosti, lakini hakuna samani. Mkoa umeshaleta mahitaji ya samani katika Wizara zinazohusika, tunaomba samani zipelekwe ili kusudi hizi shule ziwe tayari kuwapokea, hata itapunguza ile backload niliyosikia asubuhi wanasema kwamba, watoto 20,000 wamekosa kwenda form five kwa sababu, hakuna miundombinu. Pale miundombinu ipo, kinachohitajika ni samani.

Mheshimiwa Spika, Madiwani ni watu wa muhimu sana. Madiwani ni viongozi wenzetu ambao ndiyo wako karibu na wananchi. Wale kila siku wanazunguka kwenye Kata, wanapanga mambo ya maendeleo, wanaibua miradi, wanachangia maendeleo, wao wanatoa huduma za jamii, wao magari yao na pikipiki zao ndiyo zinasomba.

Mheshimiwa Spika, tunaomba kwa sababu ya hali ya maisha, posho ya Madiwani ipandishwe au ikiwezekana walipwe mishahara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namalizia kwa kusema hii bajeti ni nzuri, inawalenga Watanzania walio wengi na hasa Watanzania wenye kipato cha kawaida.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa na mimi nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri ambayo inafanywa katika Taifa hili na hasa ukizingatia kwamba yeye ndiyo msimamizi wa kazi na shughuli zote za Serikali ndani ya Taifa hili chini ya uongozi thabiti wa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Nawashukuru sana kwa sababu tumeyaona mambo makubwa yaliyofanyika na mafanikio makubwa ambayo tumeyapata kwenye elimu, afya, madini, nishati na kadhalika. Vilevile nawapongeza Mawaziri, Naibu Mawaziri, Katibu Wakuu na watendaji wote ambao wanafanya kazi chini ya Wizara hii kwa uandishi mzuri wa hotuba hii na utekelezaji uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye hotuba hii ukurasa wa 60, Serikali imefanya jambo moja kubwa zuri ambapo imewatambua wazee wetu kwa kuwapatia vitambulisho ili waweze kutibiwa bure. Wazee wetu hawa ndiyo wamejenga Taifa letu, wakiwa vijana wametumia nguvu zao na rasilimali zao kulijenga Taifa hili. Sasa hivi wamezeeka, wameishiwa nguvu, magonjwa yanawaandama kila kukicha, hawana tena mishahara, hawana nguvu za kuweza kutengeneza au kufanya kazi za kuzalisha mali kwa hiyo hawana hela ya kujitibia. Kwa hiyo, huu mpango mzuri wa Serikali wa kuwatambua wazee na kuwapa vitambulisho watibiwe bure ni mzuri na naupongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ukurasa wa 60 wanasema hadi sasa wazee ambao wameshapewa vitambulisho ni 1, 042,329. Naomba Serikali iongeze kasi kuwatambua wazee ili ifikapo mwisho wa mwaka huu basi wazee wote wawe wameshatambuliwa na waweze kupewa vitambulisho watibiwe bure katika nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu, wote tunatambua kwamba katika Tanzania kwa miaka mingi ijayo sekta ya kilimo itaendelea kutoa ajira kwa watu wengi zaidi kuliko sekta nyingine yoyote ile lakini sasa hivi tunaandaa viwanda ambavyo vinategemea kupata malighafi kutoka kwenye sekta hii. Vilevile tunamuona Waziri Mkuu anavyojitahidi kuboresha na kuongeza tija katika mazao ya kimkakati ikiwemo kahawa, pamba, tumbaku, chai pamoja na korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uzalishaji umeongezeka lakini pamoja na kazi nzuri ambayo imefanyika, tatizo tunalolipata ni masoko. Wote tunakumbuka mwaka juzi tuliona kilichotokea kwenye mbaazi, tatizo lilikuwa ni masoko. Wote tumeona kilichotokea mwaka jana kwenye kahawa na korosho tatizo ni soko na kwenye mahindi kuna wakati yalizalishwa yakakosa soko bei ikawa ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaangalia haya mazao ya kimkakati mengi yanauzwa nje, kwa hiyo, bei ya dunia ikishuka kidogo tu, huku inakuwa ni kiama kwa sababu bei kwa mkulima inaporomoka sana, mkulima anapata hasara. Kwa hiyo, napendekeza kwa Serikali kwa kuwa haya mazao ya kimkakati yanategemea bei kutoka nje, basi Serikali ianzishe mfuko ambao unaitwa Crops Price Stabilization Fund wa kumfidia mkulima kusudi hata kama bei ya dunia ikianguka, mkulima asipate hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili siliongelei mara ya kwanza, ni mara kadhaa nikiwa nachangia nalizungumza, wenzetu nchi za nje kama mkulima kukitokea natural disasters bei ikateremka kunakuwa na ruzuku anapewa kusudi asipate hasara. Nasi tuweke mfuko, mwaka huu korosho wamesaidiwa na Rais lakini tukiwa na mfuko unaoeleweka utasaidia kwenye kila zao ambalo bei zitakuwa zimeporomoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa Botswana nilizungumza na mtaalam mmoja nikitaka kujua wao wanawezaje, wao ni wafugaji kama sisi lakini nyama wanauza nje na wanapata hela za kigeni nyingi sana kutokana na mauzo ya nyama. Wakaniambia kwamba siyo kazi rahisi, hawakurupuki tu kwenda kuuza nje, wanaandaa tangu ndama wamemlishaje, wametumia viuatilifu na vyakula gani mpaka wanapokwenda kuuza wanakuwa na masoko tayari, wanazalisha kufuatana na hitaji la soko. Tujiulize tunavyopata matatizo katika kuuza mazao yetu, je, sisi tunapokuwa tunazalisha kahawa, pamba na korosho kuna soko tunalo-target, tumejiandaa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali kwa kutumia idara ambazo zinahusika na masoko waende huko nje watafute masoko. Watafute nchi marafiki zetu, waingie mikataba nao, watafute mashirika makubwa waingie mikataba nao kusudi tujue kwamba korosho au kahawa ya mtanzania tukishaizalisha tutaenda kuiuza wapi. Vilevile tuandae wakulima waanze kuandaa mazao yao kufuatana na mahitaji ya soko, tusiwaache wakalima vyovyote vile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano wa Mkoa wa Kagera. Tunao watu ambao wanauza kahawa nje lakini unakuta wanawalea wale wakulima tangu zao linapoanza, ule mbuni wanalea kwa mwaka mzima, mbolea gani utumie na mbolea gani usitumie, viuatilifu (insecticides) gani utumie na vipi usitumie, kusudi unapokuwa umezalisha ile kahawa iwe inakubalika kwenye soko lile ulilolilenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza kwamba sasa tuanze kuwalea wakulima kwa maana ya uzalishaji, tuwezeshe zile taasisi zinazofanya tafiti tuwape fedha kusudi waweze kufanya utafiti wazalishe mbegu bora, wakulima wazipande, tuweke mbolea ya kutosha kwa sababu Tanzania hatutumii mbolea ya kutosha, tuzalishe mazao bora kusudi mwisho wa siku mkulima aweze kupata bei inayofaa kwa sababu tutakuwa tumepata mazao bora. Nasisitiza ni kazi ya Serikali kuwahakikisha kwamba wanatafuta masoko kwa ajili ya mazao ya mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana ya msimu wa kahawa kwa Mkoa wa Kagera utaanza mwezi ujao wa Mei. Tunaomba Serikali ile mikakati ambayo sasa inapangwa iweze kupelekwa kwa wadau waielewe mapema kusudi tusije tukapata matatizo kama tuliyoyapata kwenye msimu uliopita. Vilevile direct export inaruhusiwa, hawa ni wanunuzi binafsi lakini Serikali isitoe kabisa mkono wake, ihakikishe kwamba inaweka bei elekezi kusudi hawa wanunuzi binafsi wasije wakawanyonya wakulima wakawapa bei ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa namalizia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mshashu.

MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha vizuri, lakini vilevile nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kazi kubwa nzuri inayoonekana ndani ya Sekta ya Afya. Wote ni mashuhuda tumeona bajeti ya afya ilivyopanda juu, wote tumeona hospitali nyingi kwa wakati mmoja zikijengwa za ngazi ya wilaya, lakini wote tumeona vituo vya afya zaidi ya 300 vinajengwa kwa wakati mmoja ndani ya Tanzania, wote tumeona tunavyonufaika na upatikanaji wa dawa ambayo sasa hivi huko zaidi ya asilimia 94, lakini wote tumeona huduma za matibabu ya kibingwa zinavyopatikana pale Muhimbili, Moi, Jakaya Kikwete, Benjamini Mkapa na Ocean Road. Tunasema hongera sana, Wizara wanafanya vizuri sana, sekta ya afya inafanya vizuri sana, kwa hiyo tunampongeza Jemedari wetu Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ya kuboresha afya ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukiangalia Mkoani Kagera tulikuwa na hospitali kumi na nne, hospitali kumi na nne kati ya hizo kumi na mbili zilikuwa za mashirika ya dini, moja ya binafsi tulikuwa na hospitali mbili tu za Serikali, lakini katika muda mfupi kwenye bajeti iliyopita wametupatia bilioni nne na nusu tunajenga hospitali za wilaya tatu na kwenye bajeti hii naona wanatuongezea mbili, tunasema ahsante sana. Vile vile, tulikuwa na vituo vya afya 34 na kati ya hivyo ni vituo vitano tu vilivyokuwa na theatre ambazo zingeweza kuwasaidia akinamama wanaopata uzazi kinzani, wameshatupatia bilioni 5.9, tumekarabati vituo vya afya 14 ambavyo vitaongeza utoaji wa huduma nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za matibabu ni kubwa mno, hakuna mtu anayeweza kuzimudu kirahisi, ndiyo maana tunasema bima ya afya ndiyo mkombozi, hata ukienda kwenye nchi za wenzetu walioendelea kitu cha kwanza wanahakikisha kwamba binadamu yeyote anakuwa na bima ya afya. Ukija kwa Tanzania kwa bahati mbaya mpaka sasa hivi watu walio kwenye mfumo wa afya wa bima ya afya ni asilimia 33 tu. Kwa hiyo, ina maana kwamba zaidi ya asilimia 60 hawapo kwenye mfumo wowote wa bima ya afya. Ni asilimia moja wanatumia bima za afya za binafsi, asilimia saba wanatumia Bima ya Afya ya Taifa na asilimia 25 ndiyo wako kwenye Bima ya Afya ya Jamii hii CHF, lakini CHF ingeweza kuwa mkombozi kwa mfano kule Mkoani Kagera kwa mtu kulipa 30 tu, anatibiwa yeye, mke na watoto wane, kwa hiyo watu sita wanatibiwa kwa elfu 30 kwa mwaka mzima na katika kituo chochote kile katika mkoa. Kwa hiyo hii naona kwamba ndiyo imekuwa mkombozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoiomba Wizara ingeweka mkakati wa makusudi wa kuhakikisha kwamba sasa wanaenda kuhamasisha kwenye vijiji vyote kuhakikisha kwamba Watanzania sasa wanaingia kwenye hii CHF iliyoboreshwa ili waweze kupata huduma ya afya na kama tunaweza kuipandisha sasa, watu walioko kwenye CHF wakatoka kwenye asilimia 25 ya sasa, tukaenda mpaka asilimia 60, hata wanapokuja kuzungumzia Bima ya Afya kwa kila mtu itakuwa ni rahisi, watakuwa wameshazoea, wameshajua utamu wa Bima ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera inaitwa Bukoba Referral Governemnt Hospital, lakini hospitali hii ina changamoto kubwa sana. Wote mnajua Mkoa wa Kagera upo pembezoni jamani, unakwenda weee unavuka Ziwa Victoria upande ule karibu na Uganda, Rwanda na Burundi ndiyo Mkoa wa Kagera ulipo. Kwa hiyo hospitali tunayoitegemea ni hiyo Hospitali ya Rufaa ya Bukoba, lakini bado ina changamoto kibao, kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi, kati ya watumishi 6,265 wanaohitajika, wako watumishi elfu mbili mia tatu sabini na kitu ambayo ni asilimia 37.9 tu, tunaomba tupatiwe watumishi, Madaktari, Wauguzi na Madaktari Bingwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kule Mkoani Kagera hatuko kwenye grid ya Taifa kwa maana ya umeme. Kwa hiyo tunatumia umeme wa Uganda na umeme unakatikakatika, pale hospitali kuna generator ndogo sana ambayo haiwezi ku-supply umeme kwenye majengo yote. Tunaomba generator kubwa ya kutosha kuweza ku-supply umeme kwenye majengo yote ya Hospitali ya Rufaa ya Bukoba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilizungumza kwa uchungu nikiomba ambulance kwamba hospitali ile ya rufaa inayotegemewa na watu watakaoshindikana Kyerwa, Karagwe, Ngara, Biharamulo, Muleba, Misenyi na Bukoba yenyewe haina ambulance. Mtu akipata rufaa anaenda kwenye hospitali ya kanda ipo Mwanza, ni mwendo wa masaa nane mpaka kumi kwa basi. Sasa unakuta kwamba wakishakosa ambulance wanamweka mgonjwa kwenye basi pamoja nurse anamsindikiza kwa masaa hayo mpaka Bungando, ni hatari, anaweza kupoteza hata maisha. Niliomba mwaka jana Mheshimiwa Waziri aliniahidi, lakini sijapata hata Waziri Mkuu nilimwendea na mwenyewe akaahidi bado hatujapata. Tunaomba tupatiwe ambulance ili tuwasafirishe watu wanaokuwa wamezidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niishukuru Serikali kwa sababu kwa sababu hospitali ile wanatupanulia kwenye wodi ya wazazi wanaongeza theatre ili akinamama wanaopata uzazi pingamizi waweze kufanyiwa upasuaji. Hapo awali ilikuwa kama mama anapaswa kwenda kufanya operesheni anapelekwa kwenye general theatre, akikuta kuna mtu mwingine anafanyiwa operation ya magonjwa mengine, inabidi asubiri, akinamama mnaojifungua una uzazi, mtoto anataka kutoka, unasubirije? Kwa hiyo nawashukuru sana kwa kutujengea hiyo theatre, lakini basi watuletee na fedha tununue vifaa kusudi theatre hiyo iweze ku-operate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendelea kuboresha hiyo Hospitali yetu ya Rufaa ya Bukoba, tunaomba wodi ya watoto ipanuliwe, ijengwe ICU ya watoto, lakini vile vile sasa hivi kuna tatizo kubwa watu wanazaa watoto njiti, tuwekewe na vyumba vya kulea njiti. Hospitali ya Bukoba inawachanganya wagonjwa wenye matatizo ya akili ambao tunawaita vichaa pamoja na wagonjwa wa kawaida. Sasa yule ziki-charge anaweza akawaumiza na wenzake. Tunaomba tujengewe hospitali ya watu ambao wana matatizo ya kiakili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinga ni bora kuliko tiba, tunayo kada ya wahudumu wa afya ambayo wanaitwa Community Health Workers, karibu elfu kumi na tatu katika Tanzania ambao waliopata mafunzo, lakini kwa bahati mbaya mpaka sasa hivi hawajaajiriwa. Hawa wakiweza kuajiriwa kwa sababu wanakaa karibu na wananchi wanaweza kwenda kule kwa sababu wanayaelewa matatizo yaliyoko kule kwenye jamii wataamasisha ujenzi wa vyoo bora, kunywa maji safi na salama, lakini umuhimu wa kutumia vyandarua, watawafuatilia wajawazito kuhakikisha wewe mama ni mjamzito mbona hujaenda kliniki? Watawafuatilia akinamama kuwakumbusha kwenda kujifungulia kwenye vituo vinavyotoa huduma mapema, lakini vile vile wataangalia lishe na namna tunavyokula hiyo milo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwaajiri hawa tutapunguza magonjwa yanayotokana na uchafu kwa mfano kuhara, kuhara damu, kipindupindu, lakini watu watatumia vyandarua, kwa hiyo tutapunguza malaria na vilevile tutapunguza vifo vya mama na mtoto ambavyo vinatokana kwa sababu wengine hawaendi kwenye vituo vya afya. Rwanda wenzetu wamefanikiwa kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa sababu wanatumia Community Health Workers ambao kila wakati wanao akinamama kule kwenye vijiji wanawahamasisha na kuwafundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwa kutumia hawa watu tutakuwa tumepunguza gharama kubwa kwa sababu tutazuia magonjwa mengi, tutakuwa tumepunguza gharama ambayo sasa ingetumika kutibu hayo magonjwa na wote tunatambua kwamba kinga ni bora kuliko tiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri na Manaibu wote wawili kwa hotuba nzuri, lakini nawapongeza hasa kwa kuleta mpango wa bima ya mazao. Hii ndiyo itakuwa mkombozi wa mkulima kwa sababu kukiwa na majanga ya ukame, mafuriko au mashamba yakavamiwa na wadudu kama viwavi jeshi mkulima akapata hasara, hasara hii itaweza kulipiwa na hii bima ya mazao. Nawapongeza sana kwa huo mpango.

Mheshimiwa Spika, msimu uliopta Mkoa wa Kagera tulipata changamoto kubwa sana katika kuuza kahawa. Wakulima waliuza kahawa lakini hawakulipwa malipo yao, lakini na malipo yaliyotolewa ya awali yakawa madogo sana, shilingi 1,000. Ikambidi Waziri Mkuu atoke hapa aje Mkoa wa Kagera akaongea na wakulima, vyama vya msingi, vyama vikuu vya ushirika, viongozi wa Serikali, wafanyabiashara, lakini vilevile akaweza kuhakikisha kwamba wakulima wameanza kulipwa; namshukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nampongeza Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mheshimiwa Brigedia Jenerali Mstaafu Marko Gaguti, wakuu wa wilaya, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika wa Mkoa ambao wamelifanya sasa agenda ya kahawa kuwa agenda ya kudumu kwenye vikao na kila mahali wanapokaa. Matokeo yake ni kwamba sasa kwa msimu uliopita wote waliouza kahawa wameweza kulipwa, hata zile arrears tunazosema malipo ya pili wamepata angalau ni kidogo KDCU wametoa shilingi 100 kwa kila kilo, KCU wametoa shilingi 150. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo langu kubwa ambalo bado naliona; bei ya kahawa bado ni ndogo sana. Mkulima amepata kati ya shilingi 1,000 na 1,150, kitu ambacho kinamfanya anakata tamaa. Natoa ushauri kwa Serikali kwamba kwanza kabisa tafuta masoko ya kuuza kahawa, nenda nje muingie mikataba na nchi ambazo ni marafiki wakulima waweze kuzalisha kufuatana na mahitaji ya soko, waunganishe na soko waweze kuuza, waruhusu wanunuzi binafsi ambao tayari wana masoko kule nje waweze kuuza, muwape vibali mapema waende kuuza kabla Brazili na Vietnam ambao ni wakulima wakubwa hawajaingiza kahawa kwenye mzunguko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile ninaomba ukija kuhitimisha utuambie ili yasijitokeze yaliyojitokeza kwenye msimu uliopoita kwa wakulima kahawa; je, kwanza tayari mmeshapata soko la kununua kahawa mwaka huu? La pili, je, kuna utaratibu gani utakaotumika kwenye msimu huu ambao umeanza tena huu mwezi wa tano, ni utaratibu gani utakaotumia katika kuuza kahawa?

Na mwisho, mtueleze, je, bei ya kahawa itaweza kupanda angalau kutoka kwenye 1,000 hadi 2,000 kwa mwaka huu kwa mkulima wa Kagera ili aweze kunufaika?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. BERNADETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu kwa hotuba nzuri na kazi nzuri wanayoifanywa Wizarani.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera bado una vijiji vingi ambavyo havina umeme. Je, ni lini Miradi ya REA III, Mradi wa ujazilizi na wa Peri-urban itakamilishwa au kuanzwa lini Mkoani Kagera?

Mheshimiwa Spika, Wilaya nyingi hazikuunganishwa kwenye grid ya Taifa. Tunatumia umeme wa Uganda. Umeme huu umekuwa kero kwa wananchi kwani unakatika katika kila mara. Je, ni lini Serikali itarekebisha hayo matatizo ili wana Kagera wapate umeme wa uhakika?

Mheshimiwa Spika, Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, akiwa kwenye mkutano wa hadhara pale Bukoba Manispaa, alisema anampatia jukumu Naibu Waziri wa Nishati ahahakikishe matatizo ya umeme yanaisha kabisa Mkoani Kagera. Je, ni lini ahadi hii itatekelezwa?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. BERNADETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa hotuba nzuri ya bajeti na kazi nzuri inayotekelezwa na Wizara. Ukiondoa kipindi hiki ambapo dunia nzima imeathiriwa na Covid 19, sekta hii ni kati ya sekta zinazofanya kazi nzuri sana Tanzania. Hongera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera kuna mapori matano yaliyopandishwa hadhi na kuwa Hifadhi za Taifa za Burigi - Chato, Ibanda -Kyerwa na Rumanyika -Karagwe. Hifadhi hizi ni mpya, bado zinahitaji uwekezaji mkubwa ili kuweza kufikia lengo lililokusudiwa ya kuimarisha sekta hii na kuongeza pato la Taifa. Hivyo ili kuchochea ukuaji huu katika Hifadhi Mkoani Kagera napendekeza:-

(1) Tuletewe wanyama wengi zaidi ili waongezeke, wazaliane hifadhi zivutie watalii;

(2) Hifadhi hizi zijengewe miundombinu ya barabara na mageti yaongezwe, ili zipitike wakati wote;

(3) Tujenge Hoteli nzuri, makambi na Lodge za kudumu.

(4) Hifadhi zilipoanzishwa vijiji jirani hawakupatiwa elimu ya kutosha. Napendekeza viongozi na wanavijiji wapewe elimu ya Uhifadhi, Ulinzi shirikishi, ni faida gani wao watazipata kutokana na hifadhi hizi wa mkoani Kagera?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo kubwa la wanyamapori kama tembo, ngedere kuingia kwenye maeneo ya wananchi, wanaharibu mazao na kuua wanadamu. Wakulima wanapata hasara na vifo vinatokea mara kwa mara. Serikali ifanye yafuatayo: watafute njia ya kuzuia tembo kuingia katika maeneo ya wakulima ya kudumu; tutumie technologies za kilo kuwaondoa tembo hawa; wanyama waharibifu kama ngedele nyani wamezaliana sana, ni wengi vijijini, wanaharibu sana mazao ya wakulima. Napendekeza wavunwe, wapunguzwe ili kupunguza hizi athari. Tufufue kitengo cha Vermin Control Unit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango vya fidia na vya kifuta machozi ni vya siku nyingi, ni vidogo sana, havina uhalisia, virekebishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ya utalii ni sekta ya kipaumbele ya Serikali mbayo inachangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa. Sekta hii imeathiriwa sana na Covid 19. Serikali ichukue hatua za haraka kunusuru sekta hii. Tunaiomba Serikali ianzishe Stimulus Package ili kunusuru haraka sekta hii. Serikali itoe fedha kuwasaidia wafanyabiashara wenye hoteli, wasafirishaji na Wizara ili kunususuru sekta hii haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, kama nchi tuwe na Mfuko wa Dharura kuweza kutatua matatizo kama haya yakijitokeza. Mfuko uwe wa Kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iwe na mipango kabambe ya kuchochea utalii wa ndani. Kutoka viwandani, mashuleni, wakulima, wavuvi, watumishi na kadhalika, wote wahamasishwe na kuwekewa utaratibu ili washiriki. Itasaidia kuongeza namba ya watalii nchini na pato la Taifa.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu anavyoendelea kutulinda na kutubariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee, napenda kuwashukuru wanawake wa Mkoa wa Kagera walionichagua kwa kura nyingi. Nakishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi kwa kuniteua na leo hii ni Mbunge katika Bunge la Kumi na Mbili. Ahadi yangu kwao ni kwamba nitaendelea kuwatumikia wananchi wote kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango ulioletwa ni mzuri, tunachangia ili tuboreshe; na kwa sababu ya muda nitajikita kwenye eneo moja la kilimo. Lengo moja la Mpango huu ni kuchochea maendeleo ya watu. Kama tunataka kuchochea maendeleo ya watu, basi inabidi tuwekeze nguvu nyingi katika maeneo ambayo yana watu wengi na katika Tanzania tuna maana ya kilimo, uvuvi na ufugaji. Hatuwezi kupata maendeleo yanayotarajiwa kama tutaendelea kulima kwa jembe la mkono na kwa kutegemea mvua, ambacho ni kilimo cha kujikimu inabidi sasa twende kwenye kilimo cha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza, ili tuweze kunufaika na Mpango huu, kwanza, kila mkoa uhakikishe kwamba unatenga maeneo makubwa kwa ajili ya kilimo, watafutwe wawekezaji wa nje na ndani waweze kuwekeza kwenye mashamba makubwa ya kilimo. Vilevile wananchi wawezeshwe kupata mitaji kwa bei nafuu. Kwa maana kama wanapata mikopo kutoka benki, basi riba isizidi asilimia 10, iwe chini ya asilimia 10 kusudi waweze kuzitumia hizo hela kutafuta zana za kilimo bora na waweze kulima kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta zana nyingine ni ghali sana, kwa mfano, matrekta makubwa, excavators, vesta, weeder na vitu kama hivyo. Ingekuwa ni vizuri kila Halmashauri ikawa na mfuko wakanunua vifaa hivyo; vikundi vidogo vidogo na watu binafsi wakawa wanakodishwa kutoka kwenye Halmashauri, nao wakaweza kulima kilimo kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanya kilimo kikubwa inabidi vilevile tuwe na kilimo cha umwagiliaji. Kuna schemes mbalimbali humu katika Tanzania ambazo nyingine zilishakufa, tuzifufue lakini vilevile tunaweza kuanzisha nyingine mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Vituo vya Utafiti kama TARI, TACRI na vile vya usambazaji mbolea, lazima watusaidie kuhakikisha kwamba tunakuwa na mbegu bora. Kwa sababu hata ukilima shamba kubwa namna gani, kama mbegu uliyokuwanayo siyo bora, huwezi kupata tija yoyote. Kwa hiyo, tunaomba wapewe bajeti ya kutosha kusudi waweze kuzalisha mbegu zilizo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutafute wawekezaji, tuwashawishi, tuwatengenezee mazingira mazuri waweze kuwekeza kwenye viwanda vya kuongeza thamani ili kusudi yule mkulima wa Kahawa kutoka Mkoa wa Kagera asiuze kahawa ghafi; akaange, apaki, auze au asage auze; mkulima wa pamba atengeneze nyuzi auze, au atengeneze nguo ndiyo ziuzwe. Kwa namna hiyo, tutaweza kumfaidisha mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna tatizo kubwa la soko la mazao yetu. Naomba idara za Serikali ambazo zinahusika katika kutafuta masoko, waende nchi za nje, waingie mikataba, watu walime wakijua kwamba soko liko wapi. Natoa mfano wa Botswana. Wao wamefaidika sana na mifugo yao kwa sababu hata kabla hujaanza kufuga nchi inaaenda kuingia mikataba na nchi nyingine, unajua kwamba unafuga kwa standards zipi, ukisha-produce yale mazao inakuwa ni rahisi kuuza kwa sababu unajua unalenga soko gani. Isije ikawa kama ile story ya mbaazi ambapo watu walilima lakini wakakosa masoko.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi kwa Serikali kwa ajili ya…

MWENYEKITI: Kengele imeshagonga Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Ooh!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya tabianchi ni tatizo na athari zake zinaongezeka kila mwaka. Nchi zilizoendelea, zimechangia kwa kiasi kikubwa kwenye ongezeko la hewa ukaa angani, ambayo imesababisha upandaji wa joto duniani. Kwa mujibu wa makubaliano kwenye mikutano ya kimataifa, nchi hizo zilitakiwa kusaidia nchi zinazoendelea na masikini kwa kutoa utaalamu, teknolojia na fedha za kukabili athari za mabadiliko ya tabia nchi. Je Tanzania tumenufaikaje na Climate Change Green Funds?

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina miti mingi na hasa maeneo yenye mvua nyingi kama mkoa wa Kagera, miti inayosadia kunyonya hewa ya ukaa angani. Je, kama nchi na kama mkoa tumenufaikaje na Carbon Credit?

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya mvua nyingi sizizotabirika, Mto Kanoni katika Manispaa ya Bukoba hufurika kila mwaka na kusababisha uharibifu wa mali, nyumba, mifugo na hata kusababisha vifo vya watu na mifugo. Serikali iliahidi tangu Januari, 2023 kuanza kuongeza kina na kujenga kuta wenye kingo za Mto Kanoni. Ni lini fedha hizo zitaletwa ili kuondoa adha ya mafuriko ya kila mwaka?

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile maeneo ya Custom, Kafuti, Nyamkazi zinafurika sababu kina cha Ziwa Victoria huongezeka. Wakazi wa maaeneo haya wamekuwa wahanga wa mafuriko, wanafilisika kwa sababu ya vitu vyao na nyumba zao kuharibika kila mwaka sababu ya mafuriko. Kwa nini kusijengwe kuta kando kando ya ziwa kuwanusuru hawa wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Mazingira katika Halmashauri zetu hazipewi kipaumbele ili wakabiliane na athari ya mabadiliko ya tabianchi, inabidi wapewe bajeti ya kutosha. Wanashindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Napendekeza bajeti za Idara za Mazingira kwenye Halmashauri zetu, pia na bajeti ya Wizara hii iongezwe, sababu wana majukumu makubwa na mahitaji yanaongezeka sababu ya mabadiliko ya tabia nchi. Inabidi kama nchi tulione hili tatizo la mabadiliko ya tabianchi, tulipe umuhimu unaotosha, tulipe bajeti inayoridhisha na wakati wa kufanya hivyo ni sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. BERNADETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na wataalamu wote kwa hotuba nzuri lakini kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ndani ya Wizara kwa maana ya uboreshaji wa miundombinu. Tumeona madarasa mengi yakijengwa, vyuo vya ualimu vikikarabatiwa, shule kongwe zikikarabatiwa; kwa kweli kwenye upande wa miundombinu mmefanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri ya kuboresha miundombinu bado kuna matatizo makubwa mawili ambayo nitayaongelea. Kwanza, shule zimepanuka au zimeongezeka, wanafunzi wameongezeka mara dufu lakini walimu wameendelea kuwa wachache. Nataka niwahahakishie mimi kama mwalimu kwamba kwenye setting yoyote ya elimu mwalimu ni central, hata ukiwachukua wanafunzi ukaweka chini ya mti lakini ukamuweka mwalimu ambaye ana ujuzi uliokamilika yule mtoto ataelimika. Ukimchukua mwanafunzi ukamuwekea madarasa na vitabu ukamuondoa mwalimu hakuna kitu chochote kitakachoweza kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inasikitisha kuona kwamba mwanafunzi anamaliza form four kutoka kwenye shule A ana division one na division two, division three anachaguliwa kwenda high school anapelekewa kwenye shule, labda anaenda kusomea tahasusi ya PCB (Physics, Chemistry na Biology) anakuta kuna mwalimu mmoja wa Biology anasoma somo moja kwa miaka yote miwili form five na six at the end of the story mtihani anapewa ule ule kama aliyekuwa na walimu katika masomo yote matatu na mwisho anaambiwa kwamba ameshindwa kwa sababu atakuwa ameshinda somo moja tu. Huyu mtoto hawezi kwenda chuo kikuu, hawezi kwenda mahali popote anakuwa ameharibiwa maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napendekeza kwamba Serikali sasa ingeweka mkakati wa makusudi kuhakikisha kwamba wanaajiri walimu. Nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan juzi ametangaza kwamba sasa angalau tuanze na kuziba zile nafasi zile 6,000 kwa wale waliotoka kwenye ualimu kwa maana ya kustaafu au kuwa kuacha kazi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, naomba katika mazingira hayo wanapokwenda kuajiri hao walimu 6,000 waungalie Mkoa wa Kagera; hadi sasa tuna upungufu wa walimu 7,607 katika shule za msingi na tuna upungufu wa walimu 1,340 katika shule za sekondari. Huo ni mkoa mmoja, je, Taifa zima ikoje? Kwa hiyo, napendekeza kwamba kuwe na mkakati wa makusudi, vibali vitolewe, walimu waajiriwe ili wanafunzi waweze kuipata elimu tarajiwa.

Mheshimiwa Spika, tatizo la pili, kuna malalamiko makubwa sana juu ya elimu itolewayo kwamba haikidhi matarajio ya wanaoipata. Utawakuta wasomi wanalalamika, waajiri wanalalamika kwamba wanafunzi wanaowapata hawana zile stadi zinazohitajika katika viwanda na makampuni yao. Pia wahitimu na wenyewe wanalalamika kwamba elimu waliyoipata haiwapi ajira na wala haiwawezeshi kuweza kujiajiri.

Mheshimiwa Spika, napendekeza kwamba labda tungejifunza kutoka kwenye nchi ya China. China kwenye miaka 1970 walikuwa wanafahamika kwamba ni nchi maskini duniani, lakini wakagundua kwamba ili waweze kutoka kwenye huo mkwamo lazima waboreshe elimu yao. Wakafumua mfumo wao wa elimu, sasa hivi China ni ya viwanda, it’s a second largest economy in the world, vilevile ni wazalishaji wa mali mbalimbali ambazo zinasambazwa kote duniani. Hii ni kwa sababu waligundua kwamba elimu watakayokuwa nayo ni lazima iwe ni elimu ambayo inakuza ujuzi. Ili tufikie kwenye Tanzania ya viwanda lazima tubadilike, tutoke kwenye hii kufundisha general academic knowledge twende kufundisha elimu ambayo inakuza ajira na ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, China wao walirekebisha sheria zao za elimu, lakini kilichowafanya wafumue mfumo wao wa elimu ni walipogundua kwamba wanahitaji skilled labor ya kuweza kufanya kazi kwenye viwanda wakakuta kwamba huo utaalamu hawana. Tangu wabadilishe mfumo wao uchumi ukakua na kama mnavyojua sasa hivi uchumi wa China unakua kwa asilimia 10 kila mwaka, kwa hiyo wana uchumi mkubwa duniani. Serikali ikaweka fedha nyingi katika elimu, wakafanya reforms mbalimbali na wakaweza kufikia hapa walipofikia.

Mheshimiwa Spika, kitu cha kwanza walichofanya wakahakikisha kwamba elimu msingi ambayo inaenda mpaka sekondari ikawa compulsory (ni ya lazima). La pili, wakarekebisha mitaala. Mitaala yao sasa hivi 1/3 ya mtaala ndiyo inafundisha general academic knowledge, 1/3 ya mtaala wa China, elimu kuhusu fani mbalimbali zinazohitajika katika Maisha lakini 1/3 lazima huyu mtoto ajifunze kazi mojawapo ambayo inapatikana katika Serikali yake ya Mtaa kwa sababu wanategemea kwamba ataenda kuajiriwa kule. Vilevile wameanzisha kozi mbalimbali ili kufikia mahitaji ya viwanda. Kuna mahusiano na mikataba inawekwa kati ya shule na viwanda kila mwisho wa term wanafunzi wanaenda kwenye viwanda kusudi waweze kunoa ule ujuzi wao na wanafunzi kutoka kwenye familia masikini walikuwa wanalipiwa karo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, elimu ya kukuza ujuzi wanaianza mapema kabisa wakiwa kwenye junior secondary school ambapo sasa si watoto wameshapata ujuzi huu, wanapomaliza junior secondary school ambayo iko kama kwenye form two hapa wao asilimia 11.6 wanaenda moja kwa moja kwenye ajira kwa sababu tayari wana ujuzi, wanaweza kuajiriwa sehemu mbalimbali. Asilimia 88.4 hawa wanaendelea na senior secondary school lakini kati ya wale walioenda kwenye senior secondary school asilimia 47 wote wanaenda kwenye VETA na vyuo vya ufundi kusudi sasa waweze kupata ujuzi ambao unahitajika. Mwisho wa muhula wanafunzi wanaenda kwenye viwanda lakini kabla ya graduation kila mwanafunzi lazima apite kwenye internship kama tunavyoona hapa madaktari wanafanya.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa upande wa walimu ili uweze kufundisha kwenye secondary lazima uwe na angalau degree moja. Sisi hapa tunapeleka division three na there was a time tulikuwa tunapeleka hata division four. China wanapeleka wale cream ndiyo waweze kuwa walimu waje wawafundishe Watoto vizuri.

Mheshimiwa Spika, wakati wa likizo walimu lazima waende viwandani, wawasiliane na wenye viwanda na wenye makampuni wajue, je, wanachofundisha darasani ndiyo kinachohitajika? Aidha, walimu ambao wako kwenye vyuo vya ufundi ni lazima kila mwaka aende kukaa kiwandani kwa muda wa mwezi mmoja akiwa ananoa skills zake. Ili mwalimu apande cheo kama tunavyoona kwa mapolisi lazima kwanza afanye practical training kwenye kiwanda. Kama tunavyoona polisi lazima asomee vyeo na wao wanaenda wanafundishwa ndiyo wanaweza kupanda vyeo.

Mheshimiwa Spika, mwisho wanawa-expose hawawafungii, wanaenda kwenye nchi mbalimbali wanajifunza best practices halafu wakija wanaboresha mfumo wao wa elimu. Pamoja na kozo ndefu lakini wana kozi fupi za kumnoa mtu. Sisi hapa mtu akiajiriwa mpaka astaafu hajawahi kwenda kwenye kozi nyingine. Kwa hiyo, anafundisha hata elimu ambayo imepitwa na wakati, wao wana re-training, on job training na kadhalika. Ndugu zangu nasisitiza elimu ya ujasiriamali kwa China ni lazima. Kwa hiyo, nafikiri tukiiga mfano huu tunaweza tukaboresha elimu.

Mheshimiwa Spika, mwisho, naomba Wizara ya Eilimu na wote wanaohusika na mambo ya elimu wakubali kwamba kuna tatizo kwenye mfumo wetu wa elimu. Wafungue mjadala mpana kusudi Serikali, waajiri kwa maana ya makampuni na viwanda, wasomi pamoja na watunga sheria kwa maana ya Bunge tujadili tuangalie mfumo wetu kuna tatizo wapi? Kitu gani kinakosekana na tuongeze nini hiyo ndiyo itaweza kutupeleka kwenye dira yetu ya uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. BERNADETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa hotuba ya bajeti iliyoandaliwa vizuri. Nina imani kubwa juu ya kuwezesha utekelezaji mzuri wa bajeti hii, kwani ninatambua uwezo mkubwa, uthubutu, unyenyekevu na uchapa kazi walionao Waziri na Naibu Waziri. Pia naipongeza sana Kamati ya Bajeti kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya. Bajeti hii ni nzuri, imegusa maeneo mengi ya kuleta maendeleo na imelenga kutatua changamoto nyingi za wananchi. Ni bajeti ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha, naomba kupendekeza yafuatayo; ulipwaji madeni ya wazabuni ya mwaka 2011 hadi 2016. Kuna wazabuni waliotoa huduma na vyakula kwenye shule za sekondari kati ya mwaka 2011 hadi kati ya 2016, hawakulipwa. Madeni yalihakikiwa, Hazina ikasema italipa. Wazabuni waliokwenda Hazina baadhi walilipwa. Baadae Serikali ilirudisha madeni haya kwenye Halmashauri. Halmashauri hazikuweza kuyalipa sababu vyanzo vikubwa vya mapato vilihamishiwa TRA. Hawa wazabuni wamesubiri, wengine sasa ni miaka kumi wanaidai Serikali, huduma walitoa, lakini Serikali haijawalipa. Madeni yamelala kwenye Halmashauri mbalimbali nchini. Wazabuni hawa wameumia, wamefilisiwa na benki wamefililisika. Naomba na kuiishauri Serikali kuu ilipe madeni haya. Miaka kumi jamani, waonee huruma. Waziri ukija kuhitimisha naomba jibu ni lini watalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoani Kagera wakulima, wastaafu, wajasiriamali, viikundi vya wanawake na SACCOS mbalimbali walikuwa wameweka fedha zao katika Benki ya Wakulima ya KFCB. Benki hii ilifungwa na Benki Kuu mwaka 2018. Watu waliokuwa wameweka fedha zao humo, hawana makosa lakini wanateseka sababu fedha hizi zilifungiwa humo. Mheshimiwa Waziri ni lini watu hawa watarudishiwa fedha zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuomba upendeleo maalum (preferential treatment) wa kisera, kisheria, kikanuni, kiutaratibu, kikodi ili kuinua uchumi wa Mkoa wa Kagera. Mkoa wa Kagera uko takribani kilometa 1400 hadi 1500 kutoka Bandari ya Dar es Salaam. Mkoa umezungukwa na nchi nyingi kama Rwanda, Burundi, Uganda, na Sudan Kusini na DRC zinafikika kirahisi kutoka Kagera. Nchi hizi zingeweza kuwa soko zuri sana kwa Mkoa wa Kagera, lakini kwa sababu wao wana sera nzuri zaidi za kuvutia wawekezaji na biashara, basi kwao wanafanya vizuri kuliko sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya bajeti hii inaonesha kuwa Mkoa wa Kagera una wawekezaji kwenye viwanda wachache sana. Gharama kubwa za usafiri zinachangia mkoa kukosa wawekezaji kwenye viwanda na biashara, inapunguza uwezo wa ushindani kwenye masoko. Gharama kubwa za usafirishaji wa wataalam, kufuatilia vibali mbalimbali na usafirishaji wa wataalam na usafirishaji wa bidhaa zilizozalishwa ili zifikie masoko makubwa yaliyo Dar es Salaam, gharama hizi ni kubwa, haziwavutii wawekezaji kwani zinaongeza gharama za uzalishaji. Mfano mfuko mmoja wa simenti unaununua kati ya shilingi 13,000 hadi 14,000 Dar es Salaam, ikifika Kagera mfuko huo huo unauzwa kati ya shilingi 22,000 na 25,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi zilizotuzunguka zina sera na utaratibu mzuri zaidi unaowavutia wawekezaji. Nchi jirani zimetambua gharama za usafirishaji kama Non-Tariff Barrier (NTBs), hivyo wameweka utaratibu wawekezaji wanawekewa viwango vidogo vya kikodi. Matokeo yake sasa tunashuhudia wawekezaji wengine wakihama kutoka Tanzania kuhamia nchi jirani. Hata wafanyabiashara Watanzania, wengine wamevutiwa na kuhamishia mitaji yao nchi za jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mipakani mfano Mtukula, Rusumo na kadhaika, biashara zinachangamka upande wa Uganda na Rwanda, upande wa Tanzania biashara zinadorora. Sera, sheria na kanuni zao zimerahisishwa sana kiasi wafanyabiashara wanashawishika kufungua biashara nyingi kwa kasi Uganda kuliko Tanzania. Hata baadhi ya Watanzania wanapeleka biashara zao nchi jirani mfano pale Mtukula.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu mwaka 2019, Mkoa wa Kagera uliwasilisha ombi Serikalini wakiomba mkoa upewe Upendeleo maalum, wawekezaji Mkoa wa Kagera wapewe unafuu wa kikodi ili kufidia gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitolewa upendeleo huu wa kisera, kisheria, kikanuni na kikodi mkoa utashindana sawa na nchi jirani, milango ya uwekezaji na biashara itakuwa imefunguliwa, wawekezaji wataongezeka, uzalishaji kwenye viwanda utaongezeka, biashara za mpakani upande wa Tanzania zitaongezeka, mzunguko wa uchumi katika Mkoa wa Kagera utaongezeka na mapato ya Serikali yataongezeka.

Mheshimiwa Waziri wa Fedha, ombi la kuupatia Mkoa wa Kagera upendeleo maalum (preferential) lililoletwa Serikalini tangu mwaka 2019 ili kuchochea uwekezaji wa viwanda na biashara Mkoani Kagera litatekelezwa lini? Naomba jibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa mambo mazuri makubwa ambayo imeweza kutekeleza katika kipindi kifupi. Wametujengea madarasa 15,000 na kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania tumeweza kujenga madarasa mengi kiasi hicho na wanafunzi wote wameingia kwa mkupuo wote walioshinda kuingia kidato cha kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii vile vile imepunguza pressure kwa wazazi ambapo kwa kipindi hiki huwa wanahangaika kutafuta michango. Sasa hivi Serikali imepanga wanaenda kujenga shule 1,000 za Sekondari ili kuhakikisha kwamba kila Kata ambayo haikuwa na shule ya sekondari itakuwa imejengewa shule ya sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mama ametoa shilingi bilioni 30, wanaenda kujenga shule za wasichana katika Mikoa 10. Kwa hiyo, sisi akina mama mnaotuona hapa, ambao ni wasichana wa zamani, tulisoma kwenye shule za wasichana za bweni, tukalelewa, tukalindwa, tukaepukana na mimba na ndoa za utotoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita. Pamoja na kwamba tumejenga mashule mengi, lakini kwa sasa hivi tuna upungufu mkubwa sana wa walimu na hasa katika Mkoa wa Kagera tuna upungufu mkubwa. Bila mwalimu huwezi kutoa elimu bora, mwalimu ni central katika kutoa elimu bora. Bila walimu wa hisabati na walimu wa sayansi, huwezi kuwa na watalaam ambao wanaweza kuleta hiyo tecknolojia tunayohitaji kwa ajili ya uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza kwa Serikali kwamba watoe vibali walimu waajiriwe. Ila pale ambapo Serikali itakuwa haijatoa vibali, tunao walimu wengi waliohitimu wako mitaani, tunaomba vibali vitolewe kwa Halmashauri. Wawaajiri hawa walimu kwa kutumia own source kama part time teachers, watoto wetu wakasomeshwe. Itakapotokea kwamba vibali vya ajira vimetoka, hawa watimu wapewe kipaumbele cha kupewa ajira, lakini waendelee kufundisha watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu magonjwa yasiyoambukiza (noncommunicable disease) ni matatizo makubwa sana. Huko nyuma tulifikiri kwamba ni magonjwa ya matajiri, ni ya wazee, lakini sasa hivi wataalam wanatuambia, mtu yeyote yule anaweza kuugua. Hata watoto nao wameanza kuugua magonjwa kama kisukari, kansa, pumu, magonjwa ya akili, selimundu na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sasa hivi haya magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanaua Watanzania kuliko hata magonjwa kama Malaria, Corona na Kipindupindu. Hata hivyo, haya yanasababishwa na mtindo wa maisha. Tumeacha kutembea, tunakaa kwenye viti kwa muda mrefu, hatufanyi mazoezi, ulaji usiofaa; tunakula chumvi zaidi, tunakula mafuta zaidi; tunakula sukari zaidi, tunakunywa pombe kuzidi, tunavuta tumbaku, tunatumia madawa ya kulevya, tuna misongo ya mawazo na vile vile hatupati usingizi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi huko kwenye Majimbo, huyu anaanguka na pressure, huyu anakufa na kisukari, na kadhalika. Ndugu zangu, haya magonjwa yasiyoambukiza yanaweza kuzuilika. Kwa hiyo, ni jukumu la kila mmoja kudhibiti haya magonjwa. Therefore, tunahitaji ushiriki wa wadau mbalimbali, tuyape umuhimu. Ndiyo maana sisi kama Wabunge, baada ya kuona kwamba kuna umuhimu wa kila mtu kushiriki katika kudhibiti haya magonjwa, tumeanzisha mtandao wa Wabunge katika kudhibiti haya magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali ipange bajeti ya kutosha kwa Wizara ya Afya ili waweze kutekeleza afua mbalimbali za kudhibiti haya magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hata kwenye Wizara ya Michezo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niendelee kuchangia kwenye hoja ya Kamati hizi mbili, Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati ya USEMI. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya jamii, kwa hiyo mimi ni sehemu ya mapendekezo yaliyowekwa kule.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nipende kushukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hasan kwa ujenzi mkubwa sana wa miundo mbinu katika elimu na afya. Wote tumeshuhudia ujenzi mkubwa wa madarasa, zahanati, vituo vya afya hata hospitali. Tunasema Mama ahsante sana kwa sababu wewe unawajali Watanzania. Tatizo lililobaki ambalo ni kubwa sana ni tatizo la uhaba wa watumishi ambalo sasa linaanza kufunika na kufifisha kazi nzuri iliyofanywa na Serikali. Serikali imejenga majengo yake pale lakini kama hakuna watumishi inaonekana kwamba hatujapata thamani ya pesa iliyotumika.

Mheshimiwa Spika, daktari leo akifanya makosa wakati anatekeleza kazi zake athari utaziona pale pale Mgongwa ataugua zaidi au atafariki; lakini kwenye mfumo wa elimu kosa likitokea leo athari utakuja kuziona miaka kadhaa baadaye. Kwa hiyo ndugu zangu tunachokiona leo cha kushuka kwa ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya kidato cha nne ni kwa sababu, haya matokeo yanatokana na uchache wa walimu uliokuwepo kwa miaka mingi kadhaa. Pale ambapo kuna walimu wa kutosha ufaulu uko juu na pale ambapo kuna walimu wachache ufaulu uko chini. Kwa mfano, ukiangalia taarifa za ufaulu katika kidato cha nne mwaka 2022 kwenye masomo ya Historia, Geografia, Kiswahili ambapo unakuta upungufu wa walimu ni asilimia 5, 8, 24 hata ufaulu uko juu, kwa sababu unakuta kwenye Kiswahili wameshindwa asilimia nne kwenye historia wameshindwa kama asilimia 46. Hata hivyo, lakini ukienda kwenye masomo ya sayansi na hisabati huko ndio kuna kasheshe wanafunzi wengi wanashindwa.

Mheshimiwa Spika,Physics tuna upungufu wa walimu asilimia 77 na wanafunzi wameshindwa kwa 82, mathematics wameshindwa kwa asilimia 83 kwa sababu tuna upungufu wa walimu zaidi ya asilimia 71. Lakini ndugu zangu, hebu angalia sasa hivi kwenye shule zetu za kata tumeanza kupata division one, tunapata division two, tunapata division three. Ukiona shule ambazo zimeanza kutoa matokeo mazuri kama hayo ujue kwamba kuna walimu wazuri kwenye shule hizo lakini kule ambapo hakuna walimu hali ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa najiuliza hali hii ikiendelea kwa miaka kumi na tano ijayo watoto wakaendelea ku-fail mathematics, waka-fail physics, waka-fail biology, waka-fail chemistry itakuaje? Tutawakosa wana sayansi, tunawakosa wanateknolojia ambao tunawahitaji kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika,Je, hawa wanafunzi ambao wamesoma kwenye hizi shule ambazo zina walimu watatu mpaka watano badala ya kuwa na walimu kumi na tano mpaka ishirini, kwa hiyo wamesomeshwa nusu nusu maisha yao yatakuaje? Huyu mtoto anapomaliza kidato cha nne utakuta wamemuandika kwamba aliyeshinda ameandika pass na aliyeshindwa ameandika fail. Huyu ambaye hakuwa na walimu ni kweli ame-fail?

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali na wale wa Baraza la Mitihani waongeze category ya tatu, kuwe kuna pass, fail na huyu hakufundishwa; maana huyu unam-label kwamba ameshindwa miaka yake yote lakini kumbe wewe hukuweza kumpatia walimu wa kumfundisha. Kwa hiyo pamoja na kazi nzuri ambayo inafanywa ya ujenzi wa miundombinu katika afya na elimu nilikuwa na pendekeza yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sasa tungesimamisha kidogo mambo ya ujenzi. Najua kwamba bado tunacho kibarua cha kujenga majengo mengine kwenye afya na elimu kwa kuwa hayajatosha, lakini ili kusudi tusi-compromise ubora, tusimamishe kidogo ujenzi; tutumie hizo fedha ili Serikali itoe vibali, tuajiri watumishi kwenye afya na elimu.

Mheshimiwa Spika, najua Serikali haiwezi kuajiri walimu wote na watumishi wote wanaokosekana kwa kuwa tunao wengi waliosoma wako mitaani. Wengine tunawakuta mpaka kwenye maduka ya wahindi wanafanya kazi ili mradi wanapata kitu chochote cha kujikimu. Tuwaajiri hawa wote kwenye basis ya kujitolea. Wakiambiwa waende kujitolea wakakubali Serikali iwalipe posho kidogo kidogo; na pale itakapo tokea ajira basi hao wapate kipaumbele cha kwanza kuweza kupata hizo ajira; na tutakuwa tumeziba lile ombwe la kukosa watumishi na kukosa kutoa elimu bora au afya iliyo bora.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde thelathini malizia.

MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, vituo vyetu vya afya havina maji. Tumetembelea miradi mingine tumekuta kwamba wanavuna maji ya mvua. Unakuta kwenye maeneo yetu tunayo mvua lakini tunashindwa kuvuna maji lakini tunashindwa kuya-treat. Maeneo ya hospitali unakuta kuna nurse anaamka asubuhi anakwenda kwanza kuchota maji akafanye usafi halafu ndipo arudi kuja kuwahudumia watu. Maji yenyewe yanatoka kwenye visima vifupi, kwa hiyo sio safi na salama.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa napendekeza kwa Serikali, sasa hivi kila mradi wa zahanati na vituo vya afya vitakavyojengwa component mojawapo ni lazima iwe na mfumo wa maji safi na salama. Tuvune maji tutengeneze ma tank tutumie ultraviolet water disinfection tuweze ku disinfect hayo maji.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja za Kamati zote mbili. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa hotuba nzuri lakini vilevile kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu, kipenzi chetu ambaye anahangaika huku na kule kuhakikisha kwamba anatuletea maendeleo. Tumeona kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameifanya katika nyanja mbalimbali kama vile kwenye barabara, kwenye nishati, kwenye elimu, kwenye afya, kwenye maji kote tunaona kwamba tunaendelea kupata maendeleo. Na kwa kutumia hizi fedha alizozipata za mpango wa UVIKO basi akaweza kutujengea madarasa 15,000, tukaweza kupata ofisi za walimu 3,184, tukapata matundu ya vyoo 557 katika kipindi kifupi, madawati zaidi ya 47,000 na meza na viti zaidi ya 451,918. Kweli mama ameamua kutuletea maendeleo tunasema mama ahsante sana na nikweli mama anaupiga mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu upungufu wa watumishi. Kuna upungufu wa watumishi wengi na hasa katika sekta ya elimu, ambako hapa nazungumzia upungufu wa walimu. Kwa sasa mahitaji ya taifa tunahitaji walimu takribani 274,549, lakini kuna upungufu wa asilimia 37 ya walimu wapatao kama 100,958 kwenye shule za msingi, vilevile tunaupungufu wa walimu 74,743 katika shule za sekondari. Huu ni upungufu mkubwa sana, kama kweli tunataka kutoa elimu bora haiwezekani bila walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkumbuke mwaka 2012 kwamba watoto wa kidato cha pili walifeli wengi humu Bungeni palikuwa hapakaliki, Wabunge walitaka kujua kwanini wanafunzi wamefeli mpaka ikambidi Waziri Mkuu aunde tume, na tume ikaenda kufanyakazi kutafuta kwanini watoto walishindwa. Moja ya sababu waliyoiona ni kwamba, walikuta kwenye shule kuna walimu wachache sana. Kuna shule zilikuwa na walimu watatu, walimu wawili, mwalimu mmoja na hiyo ikachangia mass failure ya wanafunzi katika mtihani wa kidato cha nne mwaka 2012.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke kwamba mwanafunzi anayesoma sekondari anasoma vipindi saba na kuendelea. Kwa hiyo, unapokuta kwenye shule kuna walimu wanne, watatu, watano ujue kwamba huyu mwanafunzi hakusoma masomo yote. Kuna masomo ambayo hakuwahi kumuona mwalimu, kuna masomo ambayo syllabus ameigusagusa lakini hakusoma yote. Lakini ndugu zangu mtihani hauna huruma, mtihani uleule utakapotungwa atatungiwa uleule aliyekuwa na walimu wote katika masomo yote na akasoma syllabus nzima, atatungiwa huo huo na yule ambaye alikuwa hana walimu wa kutosha. At the end of story yule ambaye alikuwa hana walimu wa kutosha atafanya vibaya na tutam-label kwamba amefeli; na hii inakuwa ni hasara kwa mwanafunzi mwenyewe inakuwa ni hasara kwa mzazi, lakini vilevile ni hasara kwa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie, kwamba umuhimu wa mwalimu ni mkubwa sana. Hata ukiondoa vitabu vyote au ukawafanya wanafunzi wakakaa tu chini mkeka lakini ukawapatia mwalimu mzuri, hata kama unampa huyo mwalimu watoto ambao wanasema hawafundishiki au wale watukutu au wale slow learners lakini as long as kuna mwalimu mzuri hao watoto watajifunza na watafaulu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kuongeza ubora wa elimu mimi nilikuwa na pendekeza yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, Serikali itafute chanzo, ipate chanzo, iajiri walimu wa kutosha kwa wakati mmoja kusudi sasa tuweze kutoa elimu bora. Sasa hivi katika mashule mengi watoto wanapita tu kwa sababu wanasoma nusunusu sababu hatuna walimu wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera kuna upungufu wa walimu. Katika shule za msingi tunaupungufu wa walimu asilimia 48.8, na katika Shule za Sekondari tunaupungufu wa walimu asilimia 37.

Niombe basi, Serikali yangu wakati wanaajiri walimu katika Shule za Sekondari Mkoa wa Kagera tupatiwe angalau walimu elfu 2,108 ambao tunawakosa, na katika shule za msingi ambako tunaupungufu wa walimu 8,593 basi tupatiwe hao walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie kuhusu upungufu wa miundombinu. Najua Serikali imefanya juhudi nzuri sana za kuboresha kuongeza kukarabati miundombinu ya elimu lakini bado kuna upungufu wa madarasa na upungufu wa shule. Katika Mkoa wa Kagera tunamatatizo hasa katika upungufu wa High Schools. Kwa mfano, Wilaya ya Muleba ambayo inakata zaidi ya 40 tuna High Schools tatu, Misenye tatu, Kyerwa mbili, Karagwe High School moja na Bukoba Vijijini High School moja. Tunatambua kwamba hizi shule ni za kitaifa lakini unapowachagua watoto ambao niwatoka katika kaya maskini ambao wazazi wao wana uwezo mdogo unakuta wanarudi kuomba kwamba waendelee kusomea kwenye mikoa ileile kwa sababu ya zile gharama za kuwasafirisha. Kwa hiyo, ninaomba Serikali itusaidie waweze kutuongezea shule zenye High Schools waweke mkakati kuhakikisha kwamba shule zenye High Schools zinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mrundikano mkubwa wa wanafunzi shuleni. Pamoja na juhudi kubwa za kuongeza shule lakini hasa katika Wilaya ya Biharamulo ndugu zangu ni balaa. Najua hii inatokana na mafanikio makubwa ya elimu bila malipo lakini vilevile ni kwa sababu afya zetu ni njema, tunakula vizuri na tunazaa sana, kwa hiyo, tunawanafunzi wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano; kwenye shule ya Kabindi ambayo iko kwenye Kata ya Kabindi katika shule moja ya msingi kuna watoto 2,672, Muungano kuna watoto 2,366, Nyamarangara kuna wanafunzi 2,828 hiyo yote ni Biharamulo tu. Kikomakoma - Kabindi kuna wanafunzi 3,920, Munzani ambayo ipo Nyakaura kuna wanafunzi 3,992, Shule ya Nemba ambayo ipo katika Kata ya Nemba kuna wanafunzi 5,248 katika shule moja na shule ya Nyakanazi ambayo ni Nusaunga inawanafunzi 6,063.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu imagine huyu Mwalimu Mkuu anawezaje kuongoza shule ambayo ina watoto 6,063, 5,000, 4,000? Lakini pia hao walimu wana mzigo kiasi gani ambao wanafundisha? Hawa watoto ni kweli wanafundishwa au wanakwenda pale wanashinda wakicheza? Ndugu zangu mlione hili kama dharura, tusaidieni Mkoa wa Kagera hasa katika Wilaya ya Biharamulo, tujengewe shule, hasa kwa miradi wa EP4R kabla haijaisha tusaidie. SEQUIP tusaidie kusudi tuweze kujenga shule kwenye kata moja kwa mfano yenye watoto mpaka 6,000 tunaweza kujenga shule nyingine tatu ndani ya kata ili kunusuru hao watoto wasiwe wanaenda wanashinda shuleni tu wanacheza waweze kupata elimu ile iliyotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwisho; Mkoani Kagera mnatujengea chuo cha VETA kikubwa kizuri cha viwango. Sasa niiombe Serikali yangu tukamilishe kile kituo cha VETA ili kusudi kiweze kuanza kutoa elimu na wanafunzi waweze kupata elimu ya ufundi iliyotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kazi nzuri inayofanyika katika hii Wizara na kwa hotuba nzuri ya bajeti.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi anavyoendelea kuboresha sekta ya mifugo na uvuvi kwa kuwaongezea bajeti, kuwawezesha vijana na uboreshaji wa huduma za ugani.

Mheshimiwa Spika, mifugo; katika Mkoa wa Kagera shughuli kuu za uzalishaji ni kilimo, ufugaji na uvuvi. Ng’ombe wengi zaidi wanafugwa na watu binafsi. Kwa kuwa asilimia 90 ya eneo la malisho tayari limetumika, hivyo napendekeza yafuatayo: -

Kwanza, wafugaji/wawekezaji waliopewa vitalu, watenge maeneo, walime majani malisho; pili, wapewe elimu ya namna ya kulima majani/malisho; wawezeshwe kupata mbegu bora na NARCO iwezeshwe kuwa na matrekta na mitambo ya kulimia mashamba, wapewe mitambo ya kuvuna na kufunga majani ya malisho, ili sasa NARCO iwe inawakodisha wawekezaji mitambo, walime na kuuza majani ya malisho kwa wafugaji wengine hasa katika kipindi cha ukame/kiangazi.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera una Ranchi za Serikali tano, ya sita ambayo ni Mwisa II bado mchakato wake haujakamilika. Mwisa II ina ukubwa wa hekta 66,215.76. Vitalu tayari vilikwishakatwa, lakini wawekezaji hawajamilikishwa. Eneo hili likianza kufanya kazi litawezesha uwepo wa kiwanda cha nyama na kiwanda cha maziwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha mchakato wa Mwisa II?

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na migogoro mingi kati ya wananchi na wawekezaji waliopewa vitalu vya NARCO, kwa sasa migogoro mingi ilikwisha na imebaki katika eneo moja la Ranchi ya Kagoma; kati ya wakulima na wafugaji hakuna amani, wameanza na kuuana. Serikali ina mpango gani wa kuwagawia wananchi/wakulima maeneo na wawekezaji wakapatiwa ili kurejesha amani katika eneo hili?

Mheshimiwa Spika, kuhusu uvuvi; mkoa una fursa nyingi za uvuvi na soko la samaki ni kubwa humu nchini na Congo, Zambia, Malawi na South Sudan. Pia kuna fursa za uwekezaji katika viwanda vya uchakataji samaki, viwanda vya chakula cha samaki, cold rooms na mitambo ya kukausha dagaa.

Mheshimiwa Spika, vilevile mkoa una maziwa madogo madogo yanayoweza kutumika, wakapandikizwa vifaranga vya sato au kambale na kuwakuza, kuwavuna na kuwauza katika soko kubwa la samaki lililopo nchini na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tunampongeza Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea mradi wa ufugaji wa vizimba katika Ziwa Victoria. Kuna maeneo mengi yanayofaa kwa ufugaji wa vizimba ambayo ni Kashenye - Missenyi, Rubafu - Bukoba Vijijini, Bumble, Ikondo, Kabasharo Kimwani, Kabunyora ya Runazi na Ikuza yakiwa katika Wilaya ya Muleba.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kuwezesha maeneo hayo kupimwa na kupatiwa vibali vyote vinavyotakiwa (Ardhi, NEMC, TAFIRI). Gharama zake ni kubwa, zingewashinda wananchi/vijana/wawekezaji wengi, lakini Serikali imezibeba.

Mheshimiwa Spika, napendekeza ugawaji wa maeneo ya kuweka vizimba uzingatie pia kuwapatia maeneo ya kufugia vijana wetu wanaoishi karibu na maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Maeneo ya Rubafu (Bukoba Vijijini) tayari mwekezaji amepatikana. Je, ni lini mchakato utakamilishwa, watu wakapewa maeneo na wakaanza kufuga samaki kwenye vizimba ili kuinua kipato cha hao wananchi na Taifa?

Mheshimiwa Spika, mwisho naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri, Katibu Mkuu kwa hotuba nzuri ya bajeti iliyobeba maudhui ya mabadiliko makubwa katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha bajeti ya kilimo kupanda kwa asilimia 29 na kuruhusu mradi mzuri, mkubwa wa kuwawezesha vijana na wanawake kunufaika na kilimo wa BBT.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mpango wa BBT awamu hii ya kwanza, vijana zaidi ya 800 wako vyuoni wanapatiwa mafunzo. Faida za mpango huu wa BBT ambapo wanawake na vijana wanufaika wa mpango huu watapata ni kama ifuatavyo; ardhi iliyopimwa, hivyo watawezeshwa kumiliki ardhi; mafunzo juu kilimo cha biashara; mikopo ya kutunisha mitaji yao. Kutakuwa na dirisha la utoaji mikopo; itaondoa unyanyapaa wa vijana kwa kilimo na vijana watalima, watapata ajira na kutajirika.

Mheshimiwa Spika, ili mradi huu uwe endelevu, napendekeza watakaohusika katika kuwagawia hao vijana na wanawake maeneo, wazingatie kutenga eneo kwa wanawake na vijana wazawa wa maeneo hayo ili kuondoa malalamiko yanayoweza kutoka kwa wenyeji wa hayo maeneo.

Pia napendekeza TAMISEMI iagize Halmashauri zote nchini zibaini na kutenga maeneo ili tuwe na benki ya ardhi ya kutosha, kusudi ifikie wakati mradi huu utakapoweza kuendeshwa katika Halmashauri zote nchini na hivyo wanufaika kuwa wengi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kilimo cha vanila kinawanufaisha watu wengi duniani huko inapolimwa, mkoani Kagera kilimo cha vanila kina zaidi ya miaka 20. Lakini hadi leo hakuna soko la uhakika. Mnunuzi ambaye tena ndiye mwanzilishi wa zao la vanila Kagera, Shirika la Mayawa wana changamoto kubwa. Vanila za wakulima walizonunua tangu mwaka 2021, baadhi ya wakulima hawajalipwa hadi Leo. Mayawa walipata mkopo wa TADB wakalipa baadhi ya wakulima na wengine hawakulipwa. Hivi sasa Meneja wa Mayawa bodi imemsimamisha kazi. Wakulima wanalalamika, wanaumia hawajalipwa sasa mwaka wa pili.

Mheshimiwa Spika, Mayawa wanasema wao vanila walizonunua tangu mwaka 2021 wamekosa mnununuzi na hivyo hawajauza. Hivyo katika msimu wa mwaka 2022 hawakununua vanila na hata katika mwaka wa 2023 hawatanunua vanila.

Mheshimiwa Spika, ili kuwaokoa wakulima naomba Serikali imsaidie Mayawa kutatua changamoto hii, watafutiwe mnunuzi wa vanila kavu. Katika msimu wa mwaka jana alikuwepo mnunuzi mkubwa mmoja anayeitwa NEI. Kwa sababu alikuwa peke yake aliwawekea wakulima masharti magumu ikiwemo wakulima kulazmishwa kuvuna vanila zote kwa mara moja, hata zile ambazo hazijakomaa. Mnunuzi aliwapa muda mfupi wa yeye kununua. Sasa tunaingia katika msimu wa kuvuna mwaka huu, tunaomba Serikali ihamasishe na kuwezesha upatikanaji wa mnunuzi mwingine mkubwa wa vanila.

Mheshimiwa Spika, zao hili kwa sasa linalimwa katika mikoa mingi lakini hakuna miongozo, hakuna huduma za ugani na bei ya miche bado iko juu sana. Je, ni lini Serikali italipatia zao la vanila umuhimu unaostahili na kuweza kuwasaidia wakulima kwa kutoa huduma za ugani na kwa kupitia idara ya masoko Wizarani na TANTRED kuwatafutia soko wakulima hawa?

Mheshimiwa Spika, kuhusu mbolea ya ruzuku; tunaishukuru Serikali kwa kusambaza mbolea katika msimu uliopita. Mkoa wa Kagera ni kati ya mikoa ambayo matumizi ya mbolea bado yako chini sana. Mbolea iliyopelekwa mkoani Kagera kiasi kikubwa ilienda Kagera Sugar kwenye kilimo cha miwa. Mawakala wa usambazaji mbolea ni wachache mkoani kwani wanaogopa wasije wakaleta mbolea, ikakosa mnunuzi.

Naiomba Serikali kwenye maeneo na mikoa mingine kama Kagera ambapo wananchi matumizi yao ya mbolea yako chini, uhamasishaji juu ya matumizi sahihi ya mbolea na Serikali iwasambazie mbolea hadi kwenye vituo mbalimbali mkoani ili wakulima waipate mbolea kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, tunaipongeza Serikali kwa kuwapatia pikipiki Maafisa Ugani wote 342 walio katika mkoa wa Kagera. Hii itawawezesha kufanya kazi zao vizuri. Mkoani Kagera kuna upungufu mkubwa wa Maafisa Ugani, wapo 342 kati ya 732 wanaotakiwa. Tunaomba kupatiwa Maafisa Ugani wa kutosha waweze kusimamia na kutoa huduma za ugani kwa wakulima wa mazao mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, nampongeza Waziri wa Afya, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Wakurugenzi kwa kazi nzuri inayoendelea kufanywa katika kuboresha afya za Watanzania, mnafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa jinsi alivyoziwezesha hospitali zetu kupata ICU, Emergency, Ct- Scan, MRI, Angio Suite, Pet Scan na vifaa tiba vingine vingi. Nchi yetu sasa imeanza kupokea wagonjwa kutoka nchi nyingine sababu huduma za afya nchini kwetu zimeboreshwa sana. Ahsante sana Rais wetu na mama yetu mpendwa.

Mheshimiwa Spika, kilio kikubwa kilichopo kwenye vituo vya afya na zahanati ni upungufu wa watumishi na ukosefu wa dawa. Wananchi watafurahia uwepo wa majengo mazuri katika vituo vya kutolea huduma za afya kama wakienda kutibiwa watapata huduma nzuri ikiwemo kupata madawa stahiki. Kwa sasa upatikanaji wa dawa ni shida. Ili kuimarisha upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma ya afya, inabidi MSD ipewe nguvu na mtaji wake.

Mheshimiwa Spika, MSD inahusika na kununua, kuhifadhi na kusambaza dawa. Lakini MSD haina mtaji wa kwake wa kiwezesha kuagiza dawa mapema. Inategemea ipate bajeti ya hospitali na vituo vingine vya kutolea huduma ya afya, ndipo waanze kuagiza data. Utaratibu huu unafanya upatikanaji wa dawa unachelewa, sababu taratibu za manunuzi zinachukua miezi mitatu hadi sita. Kuna marekebisho makubwa yamefanyika ndani ya MSD, ikiwemo hata kurekebisha muundo. Ili kuisaidia MSD iweze kuzifikisha dawa mapema kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na ili MSD iweze kujiendesha kibiashara, napendekeza MSD ipewe mtaji wake yenyewe. Wakiwa na mtaji wataweza kuagiza madawa mapema na hivyo vituo ikiwemo hospitali, vituo vya afya na zahanati wakiagiza dawa, zitakuwa tayari ziko kwenye maghala ya MSD na hivyo dawa zitafikia vituo haraka. Mfumo wa sasa mkipeleke maoteo MSD ndipo inaanza mchakato wa kuagiza dawa na hivyo kuchelewa kuzipata. MSD wapewe mtaji wao.

Mheshimiwa Spika, pia Tanzania iliteuliwa kuweza kusambaza dawa katika nchi za SADC. Hii ni fursa, nchi yetu inabidi ijitahidi kutoikosa hii fursa. Ni hapo MSD itakapopewa mtaji wao wa kutosha wataweza kununua na kusambaza dawa Tanzania na katika nchi nyingine SADC.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera unapakana na nchi nyingine nne, ni rahisi kupata magonjwa ya kuambukiza na ya mlipuko kutoka nchi jirani kama UKIMWI, Ebola, Marbag na kadhalika. Pamoja na hayo Mkoa wa Kagera hakuna isolation centres. Napendekeza zijengwe isolation centres katika maeneo ya Bukoba - Muleba, Ngara, Kyerwa na Mutukura ambapo kuna mipaka inayopitisha na kuingiza watu wengi na hivyo kuongeza uwezekano wa kuletwa kwa hayo magonjwa ya kuambukiza na ya mlipuko.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera pamoja na kuwa pembezoni na kupakana na nchi nyingine kadhaa, bado hakuna hospitali yenye hadhi ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa. Hili nimekwishaliongelea sana na nimeahidiwa mara kadhaa lakini fedha za kujenga hospitali yenye hadhi ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera haipelekwi. Tunaomba tujengewe hospitali hiyo. Ni lini hii ahadi itatekelezwa?

Mheshimiwa Spika, bima ya afya ndiyo itakayokuwa mkombozi wa Watanzania walio wengi. Gharama za afya ni ghali, Watanzania wengi hawawezi kumudu gharama za matibabu. Ni lini sasa Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote utarudishwa Bungeni ili wananchi waweze kupata bima ya afya na waweze kutibiwa bila kikwazo cha kukosa fedha?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba; Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa maandalizi ya hotuba nzuri ya bajeti. Nawapongeza vilevile kwa sababu wametuletea bajeti nzuri ambayo inaleta matumaini kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti hii inalenga kukuza uchumi. Nataka kuanza na Mkoa wa Kagera. Mkoa wa Kagera, uchumi umeanguka, uchumi umekwenda chini sana. Ukiingia leo hii kwenye mitandao wale wakazi wa Kagera na wazaliwa wa Kagera wameunda makundi mengi, wote wanajadili hali mbaya, hali ya kuanguka kwa uchumi Mkoani Kagera. Hata wewe mwenyewe ukiwa unapita kule vijijini, ukaangalia wale watu, unaona kabisa kwamba uchumi umeenda chini na unaona kabisa kwamba umasikini umeongezeka.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu inayotoa orodha ya mikoa against GBP per capita ambalo ni pato la Taifa kwa kila mtu, inaonesha kwamba Mkoa wa Kagera sasa ni wa 23 katika Mikoa ya Tanzania Bara. Sisi tunashangaa mkoa ambao una misimu miwili ya mvua, mkoa ambao mvua wastani wake kwa mwaka ni milimita 500 mpaka 1,000. Kwa hiyo, ina maana kwamba mazao mengi yanaweza kuota, lakini unakuwa karibu kwenye mkia kiuchumi katika Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, nina uhakika Serikali inaliona hili, nina uhakika na nyie mnapita kwenye mtandao mnaona yale majadiliano yanayoendelea kuhusu Mkoa wa Kagera. Tunaomba sasa na nategemea kwamba Serikali inakwenda kuja na mkakati wa maksudi wa kuunusuru Mkoa wa Kagera. Ili kuinua uchumi wa Mkoa wa Kagera ninayo mapendekezo kadhaa.

Mheshimiwa Spika, kwanza, Serikali iwezeshe biashara ya mipakani. Kagera Region is strategical located, imezungukwa na Nchi nyingine kama vile Burundi, Rwanda, Uganda, vilevile ina mpaka kwa kupitia maji Kenya. Hata hivyo, pia ukiangalia wakazi wa East Africa ambao kuna South Sudan, Burundi, Rwanda, Kenya na Uganda population yake ni watu karibu milioni 195. Hilo ni soko kubwa sana ambalo tukilitumia vizuri tunaweza kuinua uchumi wa Tanzania na tunaweza tukainua uchumi wa Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tufungulie masoko ya mpakani pale Kabanga, Ngara kwenye mpaka wa Burundi, Rusumo kwenye mpaka wa Rwanda, Mutukula kwenye mpaka wa Missenyi, Nyakanazi, Murongo kwenye mpaka wa Kyerwa. Vilevile yako maeneo mengine kama Kashenye, Rubafu, wakiyafungua yale masoko pale, masoko makubwa ya ndizi, masoko makubwa ya mazao mbalimbali, minada mikubwa ya mifugo, utakuta kwamba tutakuwa tumefungua uchumi wa Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sasa ukienda kwenye hiyo mipaka niliyoizungumzia, upande wa nchi jirani unachangamka kibishara, lakini ukiangalia upande wetu wa Tanzania umedorora. Kwa hiyo, hapa kinachohitajika ni kuondoa vikwazo vya kikodi na visivyo vya kikodi kwenye sheria za biashara ili ziweze kuwa nzuri, ziwavutie wenzetu wapende kufanya biashara kwenye upande wa kwetu.

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu Mkoa wa Kagera uko mbali sana na Dar es Salaam. Vifaa vingi kwa mfano vya ujenzi vinatoka Dar es Salaam, kwa sababu ya umbali ule unakuta by the time ile product inafika Mkoa wa Kagera gharama imeshakuwa kubwa sana. Kwa mfano, mfuko wa cement unakwenda mpaka unafikia hata Sh.23,000 au Sh.25,000. Kwa hiyo, napendekeza Mkoa wa Kagera upewe upendeleo maalum, differential treatment kwenye sheria, kwenye sera, kwenye kanuni za kibiashara ili sasa kuweza kuvutia wawekezaji na kuwekeza nchi za jirani ili wapende kufanya na sisi biashara.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera ni mkoa wa wakulima, wafugaji na wavuvi na Mwenyezi Mungu alitujalia akatupa Ziwa Victoria. Naomba Wizara zinazohusika wawawezeshe watu waweze kufuga samaki kwenye ziwa kwa kutumia vizimba (cage fishing), lakini vilevile hata kwenye mabwawa, watuwezeshe waweke viwanda vya kuzalisha mbegu, kwa sababu hata wale wanaofuga samaki kwenye mabwawa inafika mpaka miezi tisa bado kasamaki ni kadogo kwa sababu hawana mbegu bora.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa kilimo, Mkoa wa Kagera ni namba moja kwenye kilimo cha ndizi, lakini zile ndizi hazina soko maalum ambalo linaeleweka. Kwa hiyo, unakuta wakati wa kiangazi ambapo ndizi ni nyingi, mkungu bei inaporomoka mpaka Sh.2,000. Kwa hiyo, huyu mkulima anaenda kupata hasara. Tunaomba wapewe Maafisa Ugani wafundishwe matumizi sahihi ya mbolea, mboji, samadi na mbolea za viwandani, lakini watafutiwe soko.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani mpaka leo Kagera tukaendelea kulima mazao yaleyale, kahawa, ndizi, ndizi, kahawa. Lazima tubadilike, hatuwezi kuendelea na traditional crops peke yake. Naomba Serikali waende wahamasishe, tuweze kuanzisha haya mazao mbadala, kwa mfano vanilla, michikichi, parachichi, alizeti, vyote vinaweza kuota Mkoa wa Kagera, hili linaweza likachechemua ukuaji wa uchumi ndani ya Mkoa wa Kagera. Tusiwaache watu wakalima tu. Kwanza tutafute masoko kusudi watakaokuja kulima mazao hayo walime kwa standards zinazohitajika kwenye soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya ni kwamba labda na uchumi uliendelea kuporomoka Mkoa wa Kagera kwa sababu hakuna zao hata moja la biashara ambalo lina bei nzuri. On that note, napenda nimpongeze sana na nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, nimshukuru Waziri wa Kilimo kwa juhudi zao za dhati ambazo wamezionesha. Waziri Mkuu ameenda zaidi ya mara tatu, mara nne kuangalia kama anaweza kuchechemua na kuongeza bei ya zao la kahawa. Kwanza alienda kukemea ile ya kuuza butura, kudhibiti butura, wakaondoa tozo kibao kwenye bei ya kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wametuletea mfumo mzuri wa manunuzi kupitia minada na kwa mara ya kwanza katika historia ya Mkoa wa Kagera namna iliyofanyika last time, kilo moja ya kahawa ya arabika imeweza kuuzwa kwa Sh.3,740 ambako tumezoea Sh.1,000 au Sh.1,200. Sasa hivi tulikuwa tunasubiri kuona sasa itakuwaje kwenye hii robusta ambayo ni kahawa ambayo inalimwa na wengi kama na bei na yenyewe inaweza ikapanda vilevile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa jinsi anavyowapenda Watanzania. Kwa sasa hivi ametuletea bajeti nzuri, bajeti ya wananchi, kwa sasabu pamoja na matatizo yote yanayoendelea duniani, ambayo yanatokana na athari za UVIKO na vita vinavyoendelea Ukraine huko, lakini yeye ameweza ku-inject ruzuku ya bilioni 100 kupunguza bei ya mafuta.

Mheshimiwa Spika, vilevile tumeona bajeti ya kilimo, sekta ambayo inagusa watu wengi, bajeti yake inapanda kutoka kwenye bilioni 264 kwenda kwenye bilioni 954. Mifugo bajeti yake inapanda kwa bilioni 100. Serikali imenunua boti zaidi ya 250 za kisasa zile za faida, zinaenda kupelekwa kwa wavuvi. Vilevile, wale watumishi wa Serikali ambao wamefikia hadhi ya kupewa magari wanaenda kukopeshwa na hii itaipunguzia Serikali gharama kwa bilioni 500.

Mheshimiwa Spika, vilevile amepandisha mshahara, kitu kilichowafurahisha Watanzania kima cha chini kikapanda kwa asilimia 23.5. Pia wastaafu ile hela yao ya mwisho wanayopewa ya mkupuo imepanda kutoka kwenye asilimia 23 mpaka 33.

Mheshimiwa Spika, elimu ni bure, watoto wetu wanasoma tangu awali mpaka kidato cha sita bila ada. Naishukuru sana Serikali kwa sababu bajeti hii inaenda kuondoa umaskini, bajeti hii inaenda kuongeza uchumi, bajeti hii inaenda kuongeza ajira, bajeti hii inaenda kupunguza makali ya maisha, kweli ni bajeti ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Wanataaluma wa Kemia wa Mwaka 2016
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri wa Wizara ya Afya kwa kuleta muswada huu. Muswada huu ni muhimu sana kwa sababu wote tunajua umuhimu wa kemia katika maendeleo lakini vilevile teknolojia imepanuka sana kwa hiyo kuna changamoto nyingi zinazotokana na upanuzi huo therefore huu muswada umekuja kwa muda muafaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, umuhimu wa muswada huu ni mkubwa, hii Ofisi ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa ipo siku nyingi, lakini hawakuwa na sheria yao wenyewe, walikuwa wanatumia sheria za hapa na pale kukiwa na tatizo la mambo ya mazingira basi wanatumia Sheria ya Mazingira lakini kwa kutunga sheria hii sasa tutakuwa tumemuwezesha huyu Mkemia Mkuu wa Serikali kuwa na sheria yake moja ambayo itaweza kuongeza ufanisi (principal legislation). Sheria hii ikishatungwa itaifanya maabara hii kuwa ya mwisho na ya rufaa. Hii itampa nafasi mtu ambaye hajaridhika na matokeo ambayo yametoka labda kwenye hizi maabara ndogo ndogo aweze kupata mahali ambapo anaweza akakata rufaa na akaweza kusikilizwa, kwenye maabara kama za TBS, TFDA basi kama mtu atakuwa hajaridhika huko anaweza kukata rufaa kwenye hiyo maabara. Hivyo basi, kifungu cha nne (4) kwenye Muswada huu kieleze wazi majukumu ya Mkemia Mkuu wa Serikali kusudi sasa kusiendelee kuwa na migongano ambayo ilikuwepo kati ya majukumu ya hii maabara pamoja na maabara zile ndogo ndogo zinazoshughulika na hayo mambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kifungu cha 10 kinazungumzia uteuzi wa Mkemia Mkuu na kinamtaka huyu atakayeteuliwa awe na shahada ya uzamili ya kemia au taaluma nyingine zinazofanana na hizo. Hata hivyo, tukumbuke sasa hivi vipo vyuo vingi, wengine degree tunapata tu kwenye internet, wengine tunapewa tu, ili kuondoa matatizo ambayo yanaweza kujitokeza tukakuta ameteuliwa mtu ambaye hana sifa zinazotakiwa hicho kipengele kiseme kwamba hiyo shahada ya uzamili iwe imetoka kwenye chuo kinachotambuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kifungu cha 16(4) kinachozungumzia usimamizi wa sampuli zinazopelekwa kwenye maabara kwa ajili ya uchunguzi, kinataka maabara isiwajibike kwa mabadiliko au muonekano wa sampuli utakaojitokeza wakati wa uchunguzi au hata baada ya uchunguzi.
Ndugu zangu, mkumbuke kwamba hii maabara itakuwa inapima kemikali, sumu, vinasaba, dawa za kulevya na sampuli za kesi za jinai, kwa hiyo, lazima tuwe waangalifu. Ikitokea mtendaji ambaye syo mwaminifu hiki kifungu cha 16(4) kinaweza kikatumika vibaya, ukakuta mtu unapeleka sampuli ukihisi kwamba ni sumu iende kupimwa ikapimwa lakini ukaambiwa kwamba hii haikuwa sumu ilikuwa ni chumvi au ukapeleka bhangi unakwenda kuangalia unakuta imeshakuwa mchicha. Kwa hiyo, napendekeza kwamba hicho kifungu kielezwe vizuri kusudi hao watu ambao siyo waaminifu wasiweze kukitumia vibaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, siku hizi wanaume wengi wanawapa wanawake mimba, lakini wanawakana watoto. Wengine wanawapa mimba wanafunzi, wanawatelekeza, watoto wa watu wanaishia kufukuzwa shule na kwa sababu hawawezi kupata kazi kwa hiyo watakuwa hawana kipato, wataendelea kuwa maskini na watoto wao wataendelea kuwa maskini. Pia wote tunaona ukatili kwa watoto unaongezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna takwimu zimetolewa juzi juzi na Dawati la Jinsia na Watoto katika Jeshi la Polisi ambapo wamebaini kwamba kwa mwaka huu tu tangu mwezi Januari mpaka Julai, watoto 2,571 wamebakwa. Je, wamebakwa na nani? Unaweza ukakuta hata mtu mwingine unaishi naye humo ndani ndiye mbakaji, lakini hujui. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuwabaini wanaume wanaowakana watoto, wanawapa mimba wanawake lakini wanaogopa majukumu wanawakana watoto, kuwabaini wanaowapa wanafunzi mimba na kuwabaini hao wanaobaka watoto na kuwalawiti, Maabara hii ya Mkemia Mkuu wa Serikali inaweza ikatumika au itatumika kupima DNA ambayo itakuwa ni kipimo sahihi kuonesha ni nani amefanya tukio hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ili watendaji wasije wakashawishiwa kwa rushwa kubwa au ndogo, napendekeza adhabu iongezeke ambayo iko kwenye kifungu cha 53. Adhabu kwenye kifungu hiki iongezeke ili isomeke kwamba fine isiwe chini ya shilingi milioni tano na kifungo kisiwe chini ya miezi kumi na mbili kusudi mtu aweze kupewa adhabu kubwa kufuatana na kosa atakalokuwa amelifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ipendekeze kwamba sheria hizi zikishapita basi kanuni zitungwe haraka sana kusudi hizi sheria ziweze kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijajitendea haki na nitakuwa sijawatendea haki wana Kagera, mimi kama Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kagera ambaye ni mwakilishi bila ya kulizungumzia hili ambalo limetokea Mkoani Kagera.
Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kwa kuwapa pole wenzangu wote ambao wako kule walioathirika kwa matatizo makubwa waliyoyapata ambayo yametokana na tetemeko la ardhi. Najua imetokea Kanda ya Ziwa lakini Mkoa wa Kagera umeathirika vibaya sana na hasa hasa Bukoba Mjini. Leo hii tumeambiwa watu 17 wameshafariki, tumesikia katika taarifa mbalimbali na kwamba watu zaidi ya 252 wamejeruhiwa, nyumba zaidi ya 840 zimeanguka, nyumba zaidi 1,264 zimepata nyufa kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie ukifika pale Bukoba Mjini utakuta karibu nyumba zote zina nyufa, Bukoba Vijijini nyumba nyingi zina nyufa, Misenyi, Muleba na kadhalika lakini vifaa vya ndani vimeharibika kwa kweli ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana na kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuona umuhimu wa tatizo hili na akaamua kuahirisha ziara yake ili aweze kulishughulikia akiwa hapa hapa. Namshukuru Waziri Mkuu, Mheshimiwa Majaliwa kwa upendo wake, kwa kuwajali watu na uharaka alioutumia kufika Bukoba kwenye site akaweza kuwafariji watu lakini akashiriki vilevile kwenye hatua za awali za mazishi. Niwapongeze viongozi wa Mkoa ambao wako kule kule, kuna Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi, Mstahiki Meya wa Manispaa, Madiwani, Kamati za Maafa wote hawalali sasa hivi kila mtu anahangaika afanye nini. Nimshukuru Waziri, Mheshimiwa Jenista Mhagama ambaye yuko huko kwa sasa wanapanga mipango na kuangalia wanasaidiaje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru na Wabunge wa CCM na Wabunge wa Upinzani ambao wamekwenda kule…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba Serikali iongeze nguvu ya kuweza kupeleka vitu haraka kwa sababu watu wanalala nje na mvua zimeanza.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia muswada huu.
Kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Nape, Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Anastazia Wambura, kwa kuleta muswada huu mbele ya Bunge hili, muswada ambao umesubiriwa kwa muda mrefu sana. Naipongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Peter Serukamba kwa kuweza kujadili na kurekebisha muswada huu kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, historia ya muswada huu ni ndefu sana, ina zaidi ya miaka 20. Tumeelezwa hapa, kwa mara ya kwanza muswada huu uliletwa Bungeni mwaka 1993, lakini wanahabari wakalalamika kwamba walikuwa hawajashirikishwa vya kutosha na kwamba muswada huu ulikuwa unabana uhuru wa habari, kwa hiyo, ukaondolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada huu ukaendelea kurekebishwa, ilipofika Machi, 2015 ukaletwa tena Bungeni, wanahabari wakalalamika kwamba hawajashirikishwa tena, lakini vilevile wakawa wanahoji, kwa nini umeletwa chini ya hati ya dharura, muswada ukaondolewa tena. Serikali ikaendelea kuurekebisha huu muswada, ilipofika mwaka huu mwezi wa nane, ikatangaza kwenye Gazeti la Serikali na ilipofika tarehe 16 Septemba, muswada huu ukasomwa mara ya kwanza humu Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mwezi mmoja, wadau wa habari wakaitwa mbele ya Kamati ili watoe maoni yao, wakasema hawana maoni kwa sababu muda umekuwa mfupi. Kamati ikawapa muda wa siku kumi zaidi. Baada ya siku kumi wengine wakaleta maoni lakini wengine wakaendelea kusema kwamba muda ulikuwa hautoshi wanataka mpaka Februari, 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kwa kweli mimi ilinishangaza sana kwa sababu, huu muswada umesubiriwa zaidi ya miaka 20 na hao hao wanahabari. Wanahabari wameendelea kulalamika kwamba Sheria ya Magazeti inawatesa, wamepata nafasi, muswada wenyewe wenzangu una kurasa 28 tu, mtu ambaye una interest na huu muswada utashindwaje kusoma kurasa 28 katika karibu siku 43 walizopewa ukajadili na ukaweza kutoa maoni?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo wale wale waliosema hawana maoni, wakawa wanaonekana kila siku kwenye vyombo vya habari, wanatoa maoni juu ya huu muswada kifungu kwa kifungu. Kwa sababu hii Kamati ilikuwa sikuvu, tukaendelea kuyasikiliza hata yaliyokuwa kwenye vyombo vya habari, na kwa kiwango kikubwa yote yameingizwa kwenye huu muswada ambao upo mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye vifungu. Ukiangalia kifungu cha 7(1)(b)(iv), hiki kinaonekana bado kina ukakasi kwa sababu kinazungumzia wajibu na haki ya vyombo vya habari kwamba kutangaza na kuchapisha habari au muswada ambao ni muhimu kwa Taifa kwa kadri Serikali itakavyoelekeza.
Ndugu zangu, hapa Serikali inachosema ni kwamba ikitokea kwa mfano dharura, leo hii kimekuja kimbunga kama vimbunga tunavyoona huko Amerika, inatakiwa watu wa Dar es Salaam centre pale waondolewe na kupelekwa Kibaha, au ikitokea vita mahali popote hapa Tanzania, wanategemea kwamba vyombo vyote vya habari vitakuwa vinatangaza juu ya hiyo vita; kisije kikatokea chombo cha habari wakati huo kikaendelea na programu zake za kawaida na wengine wanatangaza burudani. Kwa wakati huo watatakiwa kutangaza kitu hicho muhimu ambacho ni kwa ajili ya maslahi ya Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 7(3) kinaipa ukuu hii sheria ambayo tunaitunga sasa. Ikitokea mgongano kati ya sheria hii na sheria yoyote ile, basi hii sheria ndiyo itatumika kuamulia huo mgongano. Mimi hiki nakiona kama ni kitu kizuri kwa sababu sheria ambayo inaweza kumtetea au kutetea chombo cha habari ni hii hapa. Kwa hiyo, naona ni vizuri kiendelee kuwemo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia vifungu vya 9, 17, 10, 50(4); Kifungu cha 9 kabla ya kurekebishwa kilikuwa kinampa Mkurugenzi wa Habari uwezo wa kukataa maombi ya kutoa leseni kwa yeyote ambaye hajatimiza vigezo au kufuta leseni kama mwenye leseni atakuwa hakuzingatia masharti.
Kifungu cha 17(1) kilikuwa kinatamka kwamba Waziri ndio mamlaka ya mwisho ya nidhamu, lakini kwa sasa kifungu cha 10 kinampa uwezo mhusika ambaye hajaridhika kwenda kukata rufaa mahakamani na akasikilizwa. Kwa hiyo, wale ambao wanajadili, tusipotoshe umma, hivyo vipengele vingine vilishafutwa au vilishaondolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 56 kilimpa Mkurugenzi wa Habari au Afisa Polisi kutwaa kifaa kwa sababu kama angekuwa anaona kwamba chombo cha habari kinaendeshwa kinyume na sheria.
Kifungu cha 50(4) kilikuwa kinaruhusu mashine ya kupiga chapa iliyotumika kuchapa taarifa ya uchochezi kuchukuliwa au kuzuiliwa na Afisa wa Polisi kabla ya hata kusikilizwa. Hayo mambo yote yamefutwa tusiwadanganye Watanzania, hayapo tena kwenye muswada huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inaanzisha utaratibu, sheria hii imeweka mchakato, sheria imeweka hata na Kamati ya Malalamiko. Hivyo ukiangalia hata 56(2), wale waliokuwa wanaogopa kwamba Waziri ana mamlaka kubwa, anaweza kuamka asubuhi akafungia chombo chochote au gazeti lolote analolitaka, hayo hayapo kwa mujibu wa sheria hii tunayotunga, yote yameondolewa; kila mtu atapewa haki na mahakama. Kama hujaridhika na uamuzi wa Waziri unaweza kwenda ukakata rufaa kwenye mahakama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 18 cha Muswada huu, kinaanzisha Bodi ya Ithibati ya Wanahabari na vilevile kifungu cha 23 kinaanzisha Baraza Huru la Wanahabari. Hii sasa maana yake ni nini? ni kwamba sasa tunakwenda kuifanya tasnia hii kuwa taaluma kamili. Sasa tunakwenda kuijengea taaluma hii heshima, tunakwenda kupunguza makanjanja ambao walikuwa wanaharibu tasnia hii kwa kuandika habari ambazo ziko substandard tukiweza kuweka Bodi pamoja na Baraza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 18 kinazungumzia juu ya ithibati ya wanahabari; mtu hataruhusiwa kufanya kazi ya habari kama hatakuwa amethibitishwa na utaratibu unaowekwa na sheria hii. Nimewasikiliza waliokuwa wanaongea na nimewashangaa sana. Wanataka kutuambia kwamba katika karne hii na baada ya sayansi na teknolojia iliyokuwa mpaka kiwango hiki, mtu yeyote anayejua kufunga kidonda, tumuite daktari; mtu yeyote yule ambaye amekwenda kwenye semina ya wiki moja, akirudi kwa sababu ilikuwa inahusu sheria awe mwanasheria; na mtu yeyote anayejua kushika kalamu na karatasi akaandika aitwe mwanahabari, haiwezekani. Hii Bodi ya Ithibati lazima iwepo na wanahabari wenyewe ndiyo kitu wanachokitaka, wanataka iwe taaluma, iheshimike ili na viwango vya mishahara yao viweze kufahamika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wanapotosha, wanadanganya watu kwamba kuna kiwango cha elimu, kwamba mtu ambaye hana degree hawezi kuitwa mwanahabari. Hakuna mahali popote kwenye muswada huu yalipoandikwa hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii imetambua kwamba sasa tutakuwa na Bodi ya Ithibati, tutakuwa na Baraza Huru la Wanahabari; yote hii itakuwa na wanahabari ambao wamebobea. Watakaa chini, wataweka vigezo vya nani awe mwanahabari. Hivi vigezo vitawekwa kwenye kanuni kwa sababu ukiweka kwenye sheria, vikitakiwa kubadilishwa ni rahisi kubadilisha kanuni kuliko kubadilisha sheria.
Kwa hiyo, hivi vigezo vitawekwa kwenye kanuni. Hivyo jamani msiwadanganye watu, waache tuwaboreshee wawe na tasnia nzuri ambayo itakuwa inaheshimika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 11 kinazungumzia juu ya muundo wa bodi, hakijazingatia jinsia. Napendekeza waweke kifungu kidogo kimoja cha kuweza kuzingatia jinsia. Hebu angalia Wanahabari wote Waandamizi, karibu wote ni wanaume. Kwa hiyo, hiki kipengele kikiachwa hivi hivi unaweza ukakuta Bodi nzima ina watu wa jinsi moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, muswada huu ni mzuri, utaifanya tasnia hii kuheshimika, itakuwa ya kitaaluma, lakini kwa kupewa ithibati, kitawafanya wamiliki wa vyombo vya habari waweze kuwalipa wanahabari mshahara unaostahili na vilevile wataweza kuwakatia bima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, tumwombe Mheshimiwa Waziri baada ya sheria hii kuwa imesainiwa aharakishe kuandaa kanuni ili sheria hii ianze kutumika mara moja kwa sababu imesubiriwa kwa zaidi ya miaka 20.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma wa Mwaka 2017
MHE. BENARDETHA MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu pamoja na Wakurugenzi Wakuu wa mifuko kwa kuandaa na kutuletea huu muswada. Naipongeza sana Serikali, nimeangalia huu muswada waliotugawia leo asubuhi, naona wamezingatia maoni ya wadau pamoja na marekebisho makubwa yaliyofanywa na Kamati. Ahsanteni sana Serikali kwa kuwa wasikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada huu unalenga kuunganisha hii mifuko yote mitano tukabakia na mifuko miwili, mmoja wa Umma na mwingine wa binafsi kwa lengo la kuboresha mafao ya wafanyakazi. Kwa hiyo, ni kitu kizuri, nakiunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Ibara ya 18 ya muswada huu inayozungumzia michango kwamba mwajiri atachangia asilimia 15 ya mshahara na mwajiriwa atachangia asilimia tano; lakini ukiangalia 18(b) hii imempa Waziri mamlaka ya kuweza kubadilisha viwango kadri atakavyoona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikitokea tukawa na Waziri wakati fulani ambaye hajali wafanyakazi, unaweza ukakuta huyu Waziri ameamua kupanga kwamba contribution ya mfanyakazi iende mpaka asilimia 30. Hii inaweza ikawa shida, kwa sababu kwenye mshahara huo huo labda ukute alikuwa ni mwanafunzi anakatwa Bodi ya Mikopo, anakwata PAYE, anakatwa na vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafurahi kwamba sasa hivi kwenye kipengele hicho wamebadilisha wakasema kwamba mpaka ifanywe actuarial valuation. Sasa nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba hiyo actuarial valuation inafanywa kwenye mfuko au inafanywa kwa mfanyakazi aonekane ana nguvu kiasi gani ya kuweza kuchangia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 20 inazungumzia juu ya michango isiyowasilishwa. Hali ilivyo sasa hivi ni kwamba unakuta wastaafu wengi wanapostaafu, wanalipwa mafao kidogo sana kwa sababu michango ilikatwa kutoka kwenye mishahara yao, lakini haikuwasilishwa kwenye mifuko. Katika kipengele cha 20 kimeainisha kwamba huyu mtu sasa awe michango yake imeshawasilishwa kwenye mifuko au haijawasilishwa, mfuko utatakiwa umlipe mafao yake yote na ule mfuko wenyewe ndiyo uendelee kudaiana na mwajiri Hiki ni kitu kizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilikuwa napendekeza ilivyoandikwa pale kwenye kipengele cha 20 kinachosema; “Where the Director General is satisfied that an employee’s contribution has been deducted from his earnings, but the employer has failed to remit the contribution together with the paid employer’s contributions to the fund, he shall treat the unremitted contributions as wholly or partially paid to the purpose...” Nilikuwa napendekeza neno “partially” liondoke pale, linaleta ukakasi kusudi tuhakikishe kwamba huyu mwajiriwa atalipwa mafao yake yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 29 inazungumzia mafao atakayopata mwanachama; ni mafao saba. Naipongeza Serikali kwa sababu wameweka mafao ya yule ambaye atakuwa amestaafu, lakini vile vile kuna namna ambapo huyu hajafikia umri wa kustaafu, atafaidika. Napenda kuuliza kwamba kuna invalidity benefits ambayo inahusu watu wenye ulemavu. Ni kitu gani kitalipwa na hii mifuko ya hifadhi ya jamii na kitu gani kitalipwa na Workers Compensation Fund?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kinaitwa unemployment benefit, nawashukuru sana kwa kuliweka hili fao. Kwa mara ya kwanza katika Tanzania tutakuwa sasa tumetoa faraja kwa mtu aliyepoteza ajira. Pia naomba Mheshimiwa Waziri atufafanulie zaidi, ni kitu gani huyu mtu anategemewa kupata kwenye unemployment benefit?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 56 inazungumzia juu ya msamaha wa kodi kwenye mafao. Hii ibara imekaa vizuri kwa sababu huyu mtu amehangaika, sasa amefikia kustaafu, ukute na ile pension yake ya kila mwezi au ile gratuity anayoipata ikatwe kodi. Kwa hiyo, kipengele hiki kimesomeka kwamba huyu mtu hatakatwa kodi. Kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ila ningependa kuona, inaweza ikatokea wakatunga Sheria za Kodi ambazo zinalazimisha sasa kwamba ile pension ambayo iko kwenye sheria hii iende kukatwa kodi. Napenda kuona kwenye muswada huu au sheria hii waweke kipengele kinacholinda pension ya mfanyakazi kwamba hata zikitungwa sheria nyingine za kodi zisilazimishe pension ya mfanyakazi kukatwa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa muswada huu ni mapendekezo ya wafanyakazi na mategemeo ya wafanyakazi ni kwamba mifuko hii iunganishwe; gharama za uendeshaji zipungue, kusudi wao waweze kupata mafao makubwa zaidi. Sasa bahati mbaya kikokotoo kweli hakipo kwenye huu muswada na Mheshimiwa Waziri anasema watakiweka kwenye kanuni. Napendekeza kanuni zikishatungwa zipelekwe mbele ya Kamati itakayokuwa inahusika hizi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)