Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dua William Nkurua (11 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuongea katika Bunge lako Tukufu. Daima nitaendelea kuwashukuru na kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Nanyumbu kwa maamuzi yao ya busara yaliyosababisha mimi kuwa Mbunge wao na hatimaye ndiye mwakilishi wao katika jengo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kwa kumshukuru sana Mwenyenzi Mungu kwa kuzaliwa nchi hii ya Tanzania, ninamshukuru sana Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ni nchi ambayo Mungu aliipendelea na bado natafiti kwa nini tumependelewa hivi sijapata jibu. Nchi hii ina vivutio vikubwa duniani, sisi ni miongoni mwa watu tunaomiliki Mlima Kilimanjaro, unasifiwa kwamba ni wa pili duniani au wa kwanza Afrika, upo Tanzania lakini Tanzania hii ndio nchi ya pili duniani kuwa na vivutio vingi sana, lakini pamoja na hayo yote tukiacha mambo mengine kama Tanzanite na mambo mengine ambayo Tanzania anamiliki peke yake, dunia nzima anayo Tanzania peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mpaka sasa kwa kweli lazima tukiri hatujajipanga vizuri kutumia vitu hivi ambavyo Mungu ametupatia. Pamoja na hayo ambayo yanatajwa Wizara hii ndio ambayo kama tungeitumia vizuri, wataalam wetu wangejipanga vizuri ni Wizara ambayo ingeweza kupatia nchi hii fedha nyingi ambazo malalamiko mbalimbali ya barabara, hospitali na mambo mengine, tungeweza kutumia Wizara hii kutafuta hizo fedha na hatimaye Watanzania wakanufaika na huduma mbalimbali katika ukusanyaji wa fedha kupita Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukizungumza ukweli bado hatujakaa vizuri. Sasa kama walivyotangulia wengine kwamba Mheshimiwa Maghembe ndiyo ameanza kubeba huu mzigo, lakini hapa tutazungumza mapungufu mengi ambayo tumeona yamejitokeza kule nyuma. Mimi ni miongoni mwa watu wanaosema tunakushauri, tutakuangalia baadaye, lakini tunakushauri na utusikilize vizuri, kwa sababu kama hutatuelewa sisi nafikiri na sisi hatutakuelewa mbele ya safari, itatulazimu tuwe hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaanza kushauri Wizara hii katika eneo la kutengeneza Watanzania kupenda mazingira hasa ya hifadhi na mbuga za wanyama. Wizara yako ina jukumu kubwa la kuwafanya watu wapende mbuga za wanyama, wapende hifadhi. Watapenda baada ya kuona matunda mazuri yanayotokana na hilo. Binadamu ameumbwa kupenda mazuri na kuchukia mabaya, ukimfanyia jambo zuri mwanadamu anafurahi, ukimfanyia vibaya anakasirika ndio binadamu wa kawaida, na Watanzania wengi wako hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa watu wote ambao wamezunguka hifadhi kwa kweli wao wanajiona wako katika eneo la balaa sana. Kwa sababu mateso wanayopata wale ambao wamezunguka hifadhi ni makubwa mno utafikiri Serikali haipo. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu na Nanyumbu tuna hifadhi tunaita Lukwika – Lumesule. Hifadhi ile kila siku inakuwa yaani mipaka tunayoifahamu sisi inaongezeka. Wananchi wamepanda mazao yao lakini unashangaa unaambiwa hifadhi sasa inafika hapa. Sasa wananchi automatically wanaichukia hifadhi hata kama utawaambia kitu gani wanaichukia kwa sababu hifadhi inaongezeka siku hadi siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akitembelea kwenye Jimbo langu kwenye Kata ya Lumesule, Kata ya Napacho kwenye vijiji vya Napacho vyenyewe, Kijiji cha Mitonga na kwa ujumla ile Kata vijiji vyake wao wamezunguka hifadhi, lakini hifadhi imekwenda kukata mikorosho na kuwaambia kwamba ninyi mpo ndani ya hifadhi. Wananchi wale wanaichukia hifadhi na wanaona kwamba kuwa karibu na hifadhi ni kero. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, hakikisha kwamba mgogoro huu ambao upo kwenye Kata ya Napacho unaondolewa ili wananchi wapende hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye Kata ya Mkonona, kijiji cha Marumba na vitongoji vyake vya Namunda na Namaromba, kijiji kimesajiliwa, kina shule ya msingi, kina zahanati, kina barabara, kijiji kipo tangu Uhuru, leo wanaambiwa wapo ndani ya hifadhi. Sasa kama Serikali watu hawa imewapa miundombinu hii wamekaa hapo, watu wamehamia pale wamejenga majumba yao wanaambiwa leo wapo ndani ya hifadhi, wananchi hao wanaishi kwa mashaka. Tunawafanya watu wajisikie vibaya ndani ya nchi yao, unategemea wananchi watapenda hifadhi? Nakuomba sana Waziri, mimi nina matumaini makubwa unaweza kubadilisha hii hali. Twendeni tuwaache hawa watu waishi katika nchi yao vizuri, kama tulizubaa sisi Serikali tukawaachia watu wakae mudu mrefu ni kosa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kama tuna uwezo tutume watu wakatathimini pale walipwe fedha waondoke kama tuna uwezo, kwa sababu wananchi wako pale hawakuambiwa chochote, wamepewa Hati, kupewa Hati maana yake ni sehemu sahihi na salama kuishi. Leo unawaambiwa iko ndani ya hifadhi, huu ni unyanyasaji, kwa hiyo lazima tutengeneze mazingira rafiki na wanachi. Hilo Mheshimiwa Waziri ni eneo la kwanza ambalo nimetaka nishauri na naomba tulizingatie.
Mheshimiwa Menyekiti, eneo la pili tuwe na utaratibu mzuri wa kutoa ahadi zinazotekelezeka. Kwa mfano Wilaya ya Nanyumbu kwenye Kata hii ya Napacho kipindi hiki tarehe 8/08/2011 alitembelea Waziri wa Maliasili na Utalii kipindi hicho Mheshimiwa Ezekiel Maige. Alikwenda kijiji cha Chimika na Masuguru, alikuta pale wananchi wana shida kubwa ya maji, na shida aliyoiona kipindi kile mwenyewe akaahidi kutoa shilingi milioni sita Chimika na kutoa shilingi milioni sita Masuguru ili Halmashauri iongeze fedha nyingine wananchi wale wapatiwe maji kwa sababu na wao wamezunguka hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichotokea Mpaka leo fedha hiyo haijalipwa, Halmashauri imeandika barua nyingi hazina majibu. Sasa wananchi unapowaambia kuwa karibu na hifadhi kuna manufaa ya kuweza kupatia miradi mbalimbali na kutatua kero hawaoni.Yote haya yanasababisha wananchi wachukie hifadhi.
Ninaamini uongozi mpya wa Mheshimiwa Profesa Maghembe tutaondoa tatizo hili na hatimaye wananchi wataona faida ya kuzunguka hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuchangia eneo la utoaji wa adhabu kali kwa watu ambao wanapatikana katika maeneo ya hifadhi. Kwanza na mimi nataka niwe mmojawapo ninayekiri kwamba sipendi watu waingilie maeneo ya hifadhi, maeneo haya tumeyatunza kwa ajili yetu sisi na vizazi vinavyokuja ili Watanzania baadaye waweze kurithi huu utajiri ambao Tanzania tunao. Lakini wale watu ambao wamepata haya matatizo wameingia kule na wakaweza kushikwa wakadhibitiwa basi wapelekwe kwenye vyombo vya sheria wakapate hukumu stahiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea wananchi wanapigwa afadhali nyoka, yaani nyoka huyu mnayemfahamu ananafuu anavyopigwa kuliko anayeshikwa kule. Lakini siku zote Serikali inatangaza kwamba tuwaambie wananchi wasichukue sheria mkononi, wale wanaopigwa njiani, barabarani? Mtu anashikwa ndani ya hifadhi analetwa mpaka kijijini anapigwa anaburuzwa, hii sio sheria mkononi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mimi napowakemea wananchi jamani acheni tabia, mkimkamata mwizi msimpige, mpelekeni mahakama. Wanauliza Maliasili wakitukamata sisi mbona wanatupiga hovyo mbona hawatupeleki mahakamani? Unajibu kitu gani hapo? Mheshimiwa Waziri, una uwezo wa kuthibiti hili ondoa, askari wetu wasitumie sheria mkononi, tunajenga tabia mbaya kwa Watanzania na wao watatumia sheria mkononi, tusiwalaumu kama sisi wenyewe tunawafundisha hii tabia.
Naomba sana Mheshimiwa Waziri hii mizigo ambayo imeikuta jaribu kuiondoa na nina uhakika utakuwa na uwezo wa kuiondoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa mwisho nilitaka nijielekeze katika kuiomba Serikali kutotumia nguvu za ziada hasa kwa maeneo mengine ambayo inatia aibu. Wilaya yangu sio ya ufugaji, kwa hiyo tatizo langu tu kidogo lipo la migogoro ya wafugaji wachache waliokuja kwenye Wilaya yangu hasa kwenye Kata ya Masuguru, lakini maeneo mengi Waheshimiwa Wabunge wamelalamika humu kwamba askari wanapiga risasi ng‟ombe. Hii inaleta aibu kwa nchi yetu….
MWENYEKITI: Ahsante
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DUA W. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kabla sijaanza kuchangia katika Wizara hii nitumie nafasi hii kuishukuru sana Wizara ya Afya kwa sababu Wilaya yetu ya Nanyumbu, tangu ianzishwe tulikuwa tunafuata huduma za Hospitali ya Wilaya kwenye Wilaya ya jirani ya Masasi kwa kipindi chote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata nilipochaguliwa, wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu, miongoni mwa vipaumbele ambavyo walivitaka nivifuatilie ni kukisajili Kituo cha Afya cha Mangaka kuwa Hospitali ya Wilaya. Naishukuru sana Wizara kwa sababu baada ya kilio hiki cha siku nyingi tumewasiliana nao, tumewaeleza, mimi mwenyewe nimefanya mazungumzo nao na hatimaye sasa kwenye bajeti hii, Kituo cha Afya cha Mangaka kimepata usajili na kuwa Hospitali ya Wilaya ya Nanyumbu.(Makofi)
Mheshimiwa Waziri, naishukuru sana Wizara yako kwa niaba ya watu wa Nanyumbu, sisi ambao tulikuwa tunataabika, tunapata shida, mama zetu wanajifungua njiani kuelekea Masasi, watu wanafariki njiani kuelekea Masasi na Ndanda, kwa kweli kwa kitendo hiki tunaishukuru sana Serikali. Naomba kasi hii iendelee ili Watanzania wote katika maeneo yao walipo ambapo wanakosa hizi huduma, wapate Hospitali za Wilaya kama sisi watu wa Nanyumbu ambapo tumeshapata bahati mwaka huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo naomba nianze kuchangia. Wizara ya Afya kama walivyosema wengine, ndiyo uhai wa Watanzania. Wizara yetu inashughulika na afya za watu. Kwa hiyo, tunategemea hata watumishi kwa sababu wanagusa uhai wa watu ni lazima wawe waadilifu, lakini pia tuwajengee moyo wa kufanya kazi ili waweze kufanya kazi yao kwa ufanisi tunaoutegemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza ambayo naiona katika Wizara hii, ingawa ni vigumu sana kuijadili Wizara hii peke yake na ukaacha kuigusa TAMISEMI; changamoto ya kwanza ni kukosekana kwa zahanati za kutosha katika maeneo yetu. Kwa mfano Wilaya ya Nanyumbu ina vijiji 93, lakini tuna zahanati 17. Kwa hiyo, kuna vijiji vingi vinakosa zahanati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tuna vituo vya afya vitatu, kimoja sasa kimeshapata kuwa Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, tuna vituo vya afya viwili, tuna Kata 19. Kwa hiyo, utakuta kuna uhaba mkubwa wa majengo ya zahanati. Naiomba Wizara, ingawa jukumu hili wameliacha kwa TAMISEMI, lakini tuangalie baadaye uwezekano wa Wizara hizi mbili kukabidhiana majukumu haya vizuri. Tuwe na program ya kiuhakika ambayo itaihusisha Serikali kuu namna ya kujenga Zahanati kule vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri kamwe haziwezi kujenga Zahanati hizi ambazo tunazisema leo, haziwezi, kwa sababu mapato yao ni madogo lakini pia hata zile pesa ambazo zinatoka Serikalini kama ceiling zinakuwa pia ni ndogo. Kwa hiyo, lengo letu la kujenga zahanati kila kijiji, kama hatutajipanga vizuri, Bunge hili litamaliza muda wake tukiwa na zahanati chache sana katika vijiji vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali tuandae mpango maalum utakaoanzia Wizarani wa kupeleka pesa Halmashauri na Halmashauri pia zitenge pesa za mapato ya ndani kuongeza idadi ya zahanati kule vijijini. Mheshimiwa Waziri Ummy atakuwa ametenda kitu kikubwa sana na akinamama na wananchi wote wa Tanzania hawatamsahau. Kwa hiyo, hiyo itakuwa ni historia kubwa ambayo atakuwa ameifanya kwa kuongeza idadi kubwa ya zahanati katika vijiji vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo naiona hasa katika Wilaya ya Nanyumbu ni uhaba wa Watumishi wa Afya. Wilaya ya Nanyumbu ina uhaba wa watumishi wa afya zaidi ya asilimia 55. Kwa hiyo, utakuta sasa watumishi hawatoshi wanafanya kazi kwa nguvu kuliko uwezo wao. Hii inapelekea waichukie kazi yao; na mtu anayefanya kazi akiwa na chuki, hata lugha yake inakuwa mbovu. Tunajikuta tunawalaumu kwa sababu hawazungumzi lugha nzuri kwa wagonjwa, lakini ni kwa sababu amechoka. Mtumishi utamkuta kwenye zamu yuko mmoja, atafanya kazi mpaka jioni, usiku, mchana, muda wowote. Kwa hiyo, kwa sababu ya uchovu kuna kipindi kibinadamu anazungumza maneno ambayo mgonjwa hakutarajia ayasikie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili kukomesha hii hali, ni lazima tuongeze idadi ya watumishi hasa Nanyumbu ambako tuna upungufu wa watumishi zaidi ya asilimia 55. Kwa hiyo, hii ni changamoto kubwa katika Wizara hii ya Afya kwa sababu tuna uhaba mkubwa wa watumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Wilaya yangu kuna baadhi ya vijiji, kwa mfano Kijiji cha Marumba, Kijiji cha Maratani, Kijiji cha Mkumbaru na Kijiji cha Lumesule. Vijiji hivi zahanati zake Mganga anayetoa huduma ni Nurse; yeye ndiye anaandika dawa, yeye ndiye anayetoa dawa tunategemea nini katika hali hii? Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-windup atambue kwamba tuna changamoto hiyo na naomba atakapotaka kuwagawa watumishi katika Halmashauri atambue kwamba Nanyumbu ina upungufu wa watumishi wa zaidi ya asilimia 55.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie kuhusu CHF. CHF ni tatizo katika nchi yetu. Hatuna namna ya kuremba kwenye hili, tuna tatizo kwenye hili eneo. CHF kwanza tumewaacha wenyewe wapange kiwango gani wanafikiri wachange ili Serikali iweze kuongeza. Wengi wanachanga sh. 10,000/= wanapewa ile card na Serikali imeweka Tele kwa Tele sh. 10,000/=; jumla sh. 20,000/=.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sh. 20,000/= ingawa wanaoumwa siyo wote, lakini haiwezi ikathamini afya ya mtu, sh. 20,000/= ni ndogo sana. Kwa hiyo, nafikiri kwa sababu tunawaandaa wananchi wetu kuweza kuchangia matibabu yao wenyewe, Serikali isitoe nusu, tuwaachie wananchi watoe asilimia 30 Serikali itoe asilimia 70. Tuanzie hapo! Nafikiri tukifanya hivyo, ule Mfuko wa CHF utakuwa na pesa nyingi itakakayoweza kuwasaidia wananchi kupata huduma nzuri za afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mbunge, kwa sasa inaniwia vigumu sana kuwashawishi wananchi wajiunge na huu Mfuko kwa sababu wanakwenda hospitali wakiwa na bima yao hiyo hiyo ya CHF na hawapati dawa. Kuna kipindi inabidi uwe na moyo wa mwendawazimu kuwashawishi watu wajiunge na CHF, kutokana na hali halisi ambayo wananchi wanaiona kule hospitali. Kwa hiyo, naomba huu Mfuko tuufanyie ukarabati au tuuwekee muundo mwingine ambao utawafanya wananchi mara baada ya kujiunga wapate huduma sahihi ambayo walikuwa wanaitegemea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamechangia kuhusu MSD, sitaki nipoteze muda katika eneo hilo. MSD pia ni tatizo, naiomba Serikali ipunguze madeni huko MSD ili kile chombo kiweze kufanya kazi ambayo tunaitegemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo la On call Allowance, watu wengi wameichangia hapa. Mazingira ya watumishi wetu ni magumu lakini pia kiwango ambacho wanalipwa cha On call Allowance pia ni kidogo. Kwa mfano, katika mwaka huu wa fedha ambao tunataka tupitishe hapa, Wilaya yangu ya Nanyumbu inategemea kupata shilingi milioni tatu kwa mwezi, kwa watumishi wote hao. Hii ndiyo wapewe On call Allowance na hii zaidi ya nusu itatumika pale pale Makao Makuu ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuta kiwango hiki hakitoshi na wengine watakosa, matokeo yake tunajenga chuki baina ya watumishi na Mganga Mkuu, kwa sababu wanaamini anakula, kumbe pesa haijakwenda ya kutosha. Matokeo yake sasa wanafanya kazi wakiwa na mori mdogo na wananchi wetu wanapata shida kwa sababu hawatumikiwi na watu ambao wana moyo wa kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama kutakuwa na uwezo tuongeze kiwango hiki ambacho kitakwenda kama On call Allowance ili watumishi wetu wafanye kazi kwa moyo ili wananchi wapate huduma nzuri tunayoitegemea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka niutumie muda wangu vizuri, nataka nichangie eneo la wazee. Tulipokuwa tunanadi sera hizi tulizungumza vizuri sana kwamba tutawatumikia wazee. Nashukuru Wizara imejipanga namna ambavyo tutaweza kutoa huduma kwa wazee ikiwa ni pamoja na kuweka dirisha maalum la wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tusiishie hapo, ni kweli tuweke dirisha maalum, lakini dawa zipatikane kwa wakati ili mtu aone kweli wazee tunawajali. Maana tutawawekea dirisha, hakuna dawa, bado tutakuwa hatujafanya chochote kile. Kwa hiyo, nashauri sana Wizara kwamba kwa sababu tunataka tuwajali wazee na tumewawekea dirisha maalum, tuhakikishe kwamba na dawa zinapatikana muda wote na dawa ni bajeti ya kuwa na pesa nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza bajeti hii pia eneo la dawa ziongezwe ili wananchi wetu wapate huduma nzuri kama ambavyo Chama kiliahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. DUA W. NKURUA:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nitumie nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Nanyumbu kwa kunifanya kuwa kiongozi wao kama Mbunge na kuwa msemaji wao katika eneo hili, nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa anazofanya ambazo kila mtu mwenye dhamira ya kweli katika nchi yetu ni lazima amuunge mkono, kwa sababu analengo la kuwafanya Watanzania waishi maisha mazuri na Tanzania iwe sehemu salama ya kuishi watu. Nampongeza sana Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nianze kuchangia katika suala la elimu.
MHE. DUA W. NKURUA:
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Katika suala la elimu ni dhahiri kwamba, mkakati ambao umekuja na TAMISEMI unaonesha una dhamira ya kweli ya kupambana na hali halisi tuliyonayo sasa hasa ya mfumuko kwa watoto ambao wamezalishwa utokana na tamko na Sera ya CCM inayotamkwa kwamba, sasa elimu itakuwa bure.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali kama hii ni lazima Serikali ijipange vizuri kuhakikisha kwamba yale mambo ya ziada ambayo lazima yaongezeke Serikali ianze kuweka mkakati. Kwa sababu tuna ongezeko kubwa la watoto tutahitaji Walimu wengi, tutahitaji nyumba nyingi za Walimu, tutahitaji madarasa ya kutosha kwa ajili ya kuweza kukabiliana na hawa watoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali hii tusiziachie Halmashauri peke yake kujenga nyumba za Walimu na kuongeza madarasa, kwa sababu mapato ya Halmashauri nyingi nchini ni madogo sana. Kwa hiyo lazima Serikali ije na mpango utakaozisaidia Halmashauri kujenga nyumba za Walimu, madarasa na vifaa vingine. Waziri atakapokuja aje na mkakati akaotuonyesha kwamba tumejiandaa kukabiliana na ongezeko kubwa la watoto katika mashule yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili, ni kuhusu suala la maji, maji ni tatizo katika nchi yetu hasa katika Jimbo langu la Nanyumbu. Kutokana na hali halisi ya mazingira na uoto
tuliokuwa nao maji ni tatizo kubwa sana. Nashukuru bajeti hii imejitahidi kuonesha mikakati mbalimbali katika nchi nzima ya kupambana na shida ya maji, lakini naiomba Serikali iweke mkakati maalum na wa kipekee, kuliondoa tatizo la maji katika Mji wa Mangaka ambapo ndiyo Makao Makuu ya Wilaya na Nanyumbu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Mtwara kwa ujumla una shida kubwa sana ya maji, naomba Serikali ijipange kama ambavyo imeshatoa maelezo na nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba, wananchi wa Tanzania wanapata maji ya kutosha ili waweze kufanya shughuli zingine za kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maslahi ya Madiwani na Wenyeviti wa Halmashauri za Vijiji. Waheshimiwa Madiwani wanafanya kazi kubwa sana katika maeneo yao ya kazi, kila tatizo linalotokea katika maeneo yetu, watu ambao wananchi wanakwenda kuwafuata moja kwa moja ni Madiwani. Kwa hiyo, Madiwani ni lazima tuwatengenezee mkakati utakaowapa maslahi yatakayoweza kusaidia kukabiliana na kazi ambazo zinawakabili kwa sasa.
Naomba maslahi ya Madiwani yaangaliwe na Wenyeviti wa Vijiji walipwe mshahara. Mkakati huu lazima uanzie huku Serikali Kuu, Halmashauri hazina uwezo huu ambao tunauzungumza leo.
Naomba Serikali iwalipe Wenyeviti wa Vijiji nao ni watu wanaofanya kazi kubwa sana k
atika nchi yetu, tusipowaangalia hawa tutakuwa hatutendi haki.
Naomba suala hili tulipe kipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie asilimia 10 ambayo inapaswa iende kwa Vijana na akinamama, ni kweli Halmashauri nyingi nchini hazitengi pesa hii, hata kama zinapata mapato haya lakini hazipeleki asilimia 10 ya mapato yao. Naomba tutengeneze mpango ambao utakuwa endelevu na mpango ambao utazifanya Halmashauri ziweze kutimiza hiki kigezo, kwa sasa kuna mambo yanawashinda kufanya hii kazi ambayo tumewapa waifanye.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke kwamba, asilimia 60 ya mapato ya ndani ya Halmashauri yanatakiwa yaende kwenye miradi ya maendeleo, asilimia 20 ya mapato ya Halmashauri ya ndani yanatakiwa yaende kwenye vijiji, asilimia 10 iende kwa wanawake na vijana. Asilimia 10 peke yake maana 90 tayari tumeshazigawa, kumi peke yake ndiyo ifanye kazi zingine ikiwa ni pamoja na posho za Madiwani, kuendesha vikao na kadhalika. Kwa sababu OC ambayo ingekwenda kule kusimamia posho za Madiwani na vikao haziendi kwa wakati. Kwa hiyo, inalazimu Halmashauri zitumie pesa ambazo zingeweza
kwenda kwa akinamama na vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunataka kweli wanawake na vijana wapate pesa ni lazima Halmashauri zetu tuziongezee pesa, hii asilimia 10 tuliyowapa ni ndogo, tukumbuke kwamba Halmashauri zinalipa mchango wa ALAT-Taifa, Halmashauri zinalipa mchango wa ALAT-Mkoa, Halmashauri zinalipa loans board, asilimia 10 ile ndiyo inafanya hiyo kazi, katika hali hii unatekeleza vipi hili agizo, ni vigumu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakwenda kuwalaumu Waheshimiwa Wabunge hapa, Madiwani kule, tutawalaumu Wenyeviti wa Halmashauri, tutawalaumu Wakurugenzi lakini uhalisia haitekelezeki. Hao Madiwani ndiyo wanaosimamia hizi pesa ambazo tunazipeleka kwao, kikao hakifanyiki kwa sababu hawana pesa watasimamia vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, asilimia 10 iliyobaki haiwezi kumudu kuyafanya haya ambayo tunataka yafanyike, mazingira ni magumu sana tumewatengenezea hao watu.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana tuheshimu bajeti, hapa tunajadili bajeti na hatimaye itapita. Naomba sana mambo yatakayopitishwa hapa yafanyike hayo hayo yasiongezeke njiani wala yasipungue njiani. Tuna uzoefu wa kutosha kwamba, mara baada ya bajeti yanatokea maagizo mengine ambayo Halmashauri sasa yanawachanganya. Ni kweli maagizo yanakuwa na lengo zuri kwa mfano, tutengeneze madawati kwa watoto wetu ni jambo jema,
lakini halipo kwenye bajeti! Tunawaambia tujenge maabara ni jambo jema, lakini haikuwa kwenye bajeti. Kwa hiyo, kwa sababu haipo kwenye bajeti kinachotokea hao Waheshimiwa Madiwani na Wakurugenzi wanakwenda kuharibu mipango mingine ambayo ilipangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaambia kwamba, wao watenge asilimia 10 ya mikopo ya akinamama na vijana maana tunalalamika sana Waheshimiwa Wabunge, mikopo, mikopo, Wakurugenzi hawatengi, watatengaje wakati wameambiwa wapeleke madawati na wamepewa deadline watafanya lini!
Wameambiwa maabara tarehe fulani iishe, pale kinachoendelea mipango mingine baadaye, kipaumbele ni madawati na mabaara.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kama tunaruhusu watu waendelee kupewa maagizo nje ya bajeti, tukubaliane kwamba na asilimia 10 inaharibika tusilaumu, tunyamaze, haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, kama tumekubaliana na hii bajeti twendeni tuiheshimu. Kule Nanyumbu tunao Viongozi wa Jadi tunaita Mamwenye, wengine mnaita Machifu, wengine mnawaita Watemi. Mamwenye kwa mila yetu anaposimikwa na kufanyiwa sherehe, mtu wa kwanza kwenda kumuamkia ni Baba Mzazi na Mama Mzazi wa
yule Kiongozi. Hii ni massage kwa watu wengine kwamba, huyu anapaswa kuheshimiwa kuanzia leo. Sasa, kama kweli tunataka bajeti iheshimiwe mtu wa kwanza kuheshi
mu bajeti ni Serikali. Naomba sana Serikali tuheshimu
tutakayoyapitisha hapa ili ikatekelezwe kule kwa ufanisi ambao tumeutaka na
hapo tutakuwa tumetenda jambo jema.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo nashukuru sana na
naunga mkono hoja.
(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DUA W. NKURUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu ya TAMISEMI. Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na afya njema nikaweza kuchangia muda huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekutana hapa kuviangalia vipaumbele vya Taifa hasa katika matumizi ya pesa yetu kwa muda wa mwaka wa fedha 2017/2018. Kwa hiyo, vipaumbele vya Taifa vipo na mimi kama Mbunge nitajaribu kuviongezea vile ambavyo Wizara labda
hamkuviona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niishukuru Wizara kwa kuruhusu baadhi ya Halmshauri kutumia asilimia 60 kwa ajili ya kuendesha Halmashauri na asilimia 40 kwa miradi ya maendeleo. Suala hili kwa mtu ambaye hajadumu sana Halmashauri anaweza akaliona ni dogo, lakini Halmashauri nyingine hazina uwezo wa kuendesha Halmashauri zao. Kwa hiyo, unapowaambia watumie asilimia 60 kwa maendeleo kinachotokea ni kwamba wanakwenda kuathiri pesa zingine na cha kwanza kinachokwenda kuathiriwa ni pesa za mikopo ya akina mama na vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa kuziruhusu baadhi ya Halmashauri kutumia asilimia 40 kwenye maendeleo na asilimia 60 kuendeshea Halmashauri yao itasaidia kufuata kanuni ambazo Serikali imeweka kuliko pale mwanzo ambapo mlikuwa mnalazimisha asilimia 60 ambazo zilikuwa hazifanyi kazi. Mkumbuke hapo mwanzo ilikuwa asilimia 60 inakwenda kwenye maendeleo, asilimia 20 inakwenda kwenye vijiji na asilimia 10 ilikuwa mikopo ya vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utakuta asilimia 90 imekwenda kwenye mpango ambao Serikali imeelekeza lakini matokeo yake yalikuwa hayaendi vizuri. Kwa hiyo, hilo nalipongeza sana kwa mtazamo huo na nafikiri Halmashauri ya Nanyumbu itakuwa ni mojawapo ambayo itawekwa katika asilimia 40 ili waweze kuendesha vizuri Halmashauri yao na waweze kusimamia pesa nyingi ambazo Serikali inapeleka kule Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa kwanza naenda kujikita kwenye elimu. Nafahamu kwamba Taifa lolote ambalo elimu haijakaa vizuri, basi tutakuwa na matatizo mengi kwa sababu elimu ndiyo kama taa, ndiyo kama mwongozo wetu wa kuweza kupambana na maisha
haya ya dunia. Sasa Serikali yetu imeweka vipaumbele vingi katika elimu, imetuonesha katika Bajeti yake mambo gani ya msingi yatakwenda kuzingatiwa ili tuweze kuisimamia vizuri elimu. Sasa nayaunga mkono yote hayo na nataka nisisitize baadhi ya machache.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, Serikali iweke utaratibu wa wazi wa kuweza kuboresha miundombinu ya shule. Tuna matatizo ya madarasa, nyumba za Walimu na Walimu. Maeneo haya matatu yanatusumbua sana katika Serikali yetu. Naiomba sana Serikali isaidie Halmashauri katika ujenzi wa shule, nyumba za Walimu na vyoo katika shule zetu zote za nchi nzima. Katika eneo hili itatusaidia kuwa na shule
zenye ubora, lakini pia kuwa na Walimu wenye moyo wa kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka Serikali itilie mkazo ni malipo ya Walimu. Nimeona mkakati ambao Serikali imeuweka, naupongeza, lakini naomba sana Serikali isisitize kuhakikisha kwamba Walimu wetu wanapata malipo yatakayowasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine katika elimu ambalo naomba sana Serikali iliangalie ni uhaba wa Walimu. Wilaya ya Nanyumbu, kwa matokeo ya Darasa la Saba mwaka jana tulifanya vibaya sana katika Mkoa wa Mtwara, lakini pia hata Kitaifa hatukwenda vizuri. Sisi kama Wilaya tulikaa tukayaangalia matatizo yetu ya ndani tujue ni kwa nini tumefika hapo? Tukayabainisha na tumejipanga kukabiliana nayo. Tunayo timu kule ya watu, tunao Madiwani, tunaye Mkuu wetu wa Wilaya, anafanya kazi vizuri sana. Tunahakikisha yale matatizo ya ndani tutakabiliana nayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo matatizo ya nje ambayo lazima Serikali itusaidie. La kwanza, tuna uhaba mkubwa wa Walimu. Wilaya ya Nanyumbu inahitaji Walimu zaidi ya 1,100 lakini ina Walimu kama 600 hivi. Kwa hiyo, tuna upungufu wa Walimu zaidi ya 450. Kwa hiyo, unakuta kwamba uhaba huo wa Walimu ambao umekithiri, huwezi kuwa na wanafunzi watakaofanya vizuri. Ni sawa na timu isiyo ya kocha, haita-perform vizuri. Kwa hiyo, naomba sana Serikali katika mgao wa Walimu awamu hii ihakikishe kwamba Nanyumbu inapata Walimu wa kutosha ili tuweze kuwa na elimu bora ambayo Serikali inalenga kuifikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nilichangie ni afya. Nafahamu Wizara hii ina kazi kubwa, inasimamia afya zetu na za wananchi wetu pia. Afya inafanana na elimu. Tuna uchache wa Zahanati na Vituo vya Afya. Sera ya chama chetu ambayo ndiyo inaongoza
nchi hii, tulikubaliana kwamba tutajenga Zahanati katika kila kijiji, lakini nafahamu kwamba safari hii ni ndefu, hatuwezi kujenga leo wala kesho tukamaliza vijiji vyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri zitaweka vipaumbele wapi ikajengwe; lakini naomba sana, Serikali iweke mpango maalum utakao-support Halmashauri kukamilisha lengo hili. Halmashauri zetu nyingi hazina uwezo wa kukamilisha hili. Kwa hiyo, Serikali iweke mpango ambao utaruhusu pesa nyingi kwenda Halmashauri ili kujenga hizo Zahanati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi huo hautatusumbua sana. Wananchi wamejiandaa kujenga zahanati, tusifikiri kwamba Serikali itakwenda kujenga complete hii zahanati. Wananchi wamejitoa sasa, kwa hiyo, cha msingi ni Serikali kupeleka pesa na wananchi watajenga, pale ambapo Serikali itahitaji isaidie, tutamalizia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Serikali tupeleke pesa ambazo zita-support jitihada za wananchi katika ujenzi wa zahanati katika vijiji vyetu. Tuliahidi wenyewe; nina uhakika kwa kasi ambayo tunayo ya ukusanyaji wa mapato na seriousness ya Serikali yetu na Rais
wetu, suala hili tutalikamilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua kuna watu wanafikiri ni ndoto, lakini nina uhakika kwamba kwa kasi ya Serikali yetu na kwa kasi ya Rais wetu, suala hili litafanikiwa na wanaobisha tutakutana 2020; watahakikisha! Tutafikia pakubwa, kwa sababu pesa ndiyo itakayofanya haya na
wananchi wetu tumeweza kuwaandaa vya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitahukumiwa na wananchi wangu wa Nanyumbu kwa jinsi nitakavyohamasisha na Serikali itakavyoniletea pesa ya kumalizia majengo hayo. Kwa hiyo, naiomba Serikali tutenge pesa maalum kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati na Vituo vya
Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni watumishi. Tuna uhaba mkubwa wa watumishi wa zahanati zetu. Naomba sana Serikali ijipange kuhakikisha kwamba tunaweza kumudu kuwatuma watumishi katika zahanati zetu kwa sababu tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi katika zahanati zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nilichangie ni posho ya Waheshimiwa Madiwani. Madiwani wetu wana kazi kubwa sana na wengi hapa wamegusia namna ambavyo Madiwani wanasimamia pesa ambazo Serikali inapeleka kule. Sasa huwezi kumtuma mtu akasimamie pesa, mwenyewe amechanganyikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, posho ya Madiwani ni ndogo, sisi tulikuwa huko, tumeiona ni ndogo sana kiasi kwamba wanakosa moyo wa kuweza kusimamia vizuri pesa ya Serikali ambayo ni nyingi inayokwenda kule kwenye Halmashauri. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ihakikishe
kwamba posho ya Madiwani inapanda. Imepanda siku nyingi sana; tuliomba mwaka 2016 na mwaka huu sijaona kama imeendelea vizuri. Kwa hiyo naomba sana posho ya Madiwani izingatiwe ili tuwape motisha Madiwani hawa waweze kusimamia vizuri pesa ya Serikali ambayo inakwenda kule katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine la mwisho, ni posho pia au niite mshahara wa viongozi wetu wa vijiji. Ni eneo lingine ambalo tumelisahau. Tuna vijiji vingi nafahamu, mzigo ni mkubwa lakini twende tuanze tuwaoneshe njia. Tuna Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Vitongoji. Hao wote
wanafanya kazi katika Serikali yetu kuhakikisha kwamba wananchi wanakuwa na amani na wanakuwa na maendeleo, wanasimamia maendeleo kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali katika mipango yake ituambie namna gani inafikiria kuhakikisha kwamba wananchi hasa Viongozi wa Vijiji na Wenyeviti wa Vijiji na Watendaji wanapata posho au mshahara ili wawe na moyo wa kuweza kutumikia vizuri Serikali yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia hoja iliyotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza Wizara kwa kuainisha mambo mengi kwa ufasaha, lakini changamoto kubwa ambayo naiona ni migogoro kati ya mipaka ya hifadhi na wananchi (vijiji). Naomba Serikali ishughulikie kwa umakini sana tatizo hili. Mfano, katika Wilaya ya Nanyumbu kuna mgogoro katika vijiji vya Marumba kwenye vitongoji vya Nambunda na Namaromba na kijiji cha Mbangara Mbuyuni, kitongoji cha Wanika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakazi hawa wamekuwepo hapo kabla ya uhuru wa nchi hii lakini wananchi wamekuja kujua kuwa vitongoji hivyo vipo ndani ya hifadhi baada ya muda mrefu sana, takribani kama mwaka 2014. Hali hii inafanya wananchi kuchukia Serikali wakiamini kuwa wanaonewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ikaone hali halisi ya vijiji hivyo na ikiwezekana tuwaache wananchi ili waendelee na kazi, kuwaondoa tutawapeleka wapi? Gharama za ujenzi wa nyumba na mali mbalimbali nani atalipa? Naomba sana Serikali itatue haraka tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda ninukuu ule ukurasa wa 27 ambapo Serikali imesema; “Serikali imeamua kuweka mkazo maalum wa kuyaendeleza mazao matano ya biashara ambayo ni chai, kahawa, korosho, pamba na tumbaku. Lengo ni kuongeza mapato ya wakulima.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kabisa na wazo hili zuri la Serikali kwa sababu kama tutafanikiwa ni hakika kwamba tutakuwa tumewakomboa wananchi kwa sababu asilimia kubwa ya Watanzania wanategemea kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nina hofu katika eneo hili hasa katia zao la korosho. Ili korosho izalishwe, jambo kubwa kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba pembejeo inapatikana kwa haraka na kwa wakati jambo ambalo kwa sasa nina mashaka halitafanyika kwa sababu ili korosho zipatikane mapema ni lazima mwezi wa tano wananchi waanze kupulizia sulphur, lakini mpaka sasa mimi kama Mbunge na wananchi hatujui ni lini sulphur itapatikana, itatolewa bure kama mwaka jana au itanunuliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali haijaweka wazi namna gani wananchi watapata sulphur. Hilo ni tatizo ambalo nina uhakika lengo la Serikali ambalo limendikwa hapa halitafikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kwamba, korosho ina utaratibu wake, sisi kama wakulima wa korosho, korosho inapokwenda nje inatozwa export levy na ile export levy ina utaratibu iliwekewa, 65% ya export levy inakwenda kuendeleza zao la korosho na 35% inabaki kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Lakini mpaka leo ile 65% ya wananchi haijaenda. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba, korosho mwaka huu hazitakwenda vizuri kwa sababu pesa ambayo ingekwenda kueneza zao la korosho haijaenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baya zaidi ile ni sheria ambayo ilitungwa katika Bunge hili kwamba 65% lazima iende Bodi ya Korosho, ili ikaendeleze korosho. Kwa hiyo, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu iangalie vizuri imuambie Waziri wa Fedha apeleke pesa 65% ya hizo ambayo ni shilingi bilioni 110 iende kwa wakulima wa korosho kwa sababu ni ya kwao kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, namkumbusha Waziri wa Fedha asivunje Sheria ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea hapa inakuwa kama tunakuwa na tamaa ya hizi fedha. Na hapa nakumbuka ile hadithi ya babu yangu aliyonieleza kwamba, kulikuwa na mzee alikuwa na shida ya fedha, alipomuomba Mwenyezi Mungu akampa kuku anayetaga yai la dhahabu kwa hiyo, kila siku alikuwa anapata yai la dhahabu. Huyu mzee akaingia tamaa akaamua kumkamata yule kuku na kumkamua, ili apate mayai mengi kuku akafa na ikawa ndio mwisho wa kupata fedha, kupata mayai ya dhahabu. Sasa hii tamaa ya Serikali ya kuangalia ile pesa itauwa zao la korosho; huo ni ushauri naomba Ofisi ya Waziri Mkuu izingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni suala la maji, Serikali kweli imekusidia kuhakikisha kwamba wananchi tunapata maji safi na salama hasa katka miji mikuu na vijiji vyetu. Lakini nataka niishauri Wizara ya maji, kule Nanyumbu Serikali ilishafanya upembuzi yakinifu wa kutoa maji mto Ruvuma mpaka Mji Mkuu wa Wilaya yetu ambapo ni Mangaka. Upembuzi yakinifu ulianza 2015 mpaka leo hatujapata majibu. Sasa kwa hali hii wananchi hawajui kinachoendelea na wananchi wanataka kujua Serikali yao itawatekelezea vipi huu mradi wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali, hasa Waziri wa Maji, ninakuamini sana katika utendaji wako na nilikupeleka mpaka kwenye chanzo cha maji pale Mto Ruvuma ambako maji yatatoka kuja Mjini Mangaka. Lakini mpaka leo wananchi wanashindwa kujua kitu gani kinaendelea, naiomba Serikali ihakikishe kwamba huu mradi mkubwa wa maji ambao Serikali inataka kuuleta pale Mjini Mangaka unaufuatilia vizuri na unausimamia na hatimaye wananchi wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni umeme; umeme, kama nchi tunasema kwamba, tunatembea kwa 60% labda, vijiji veytu vinapata umeme labda 60%. Sasa hofu yangu ni kwamba hatugawi huu umeme vizuri kwa mtawanyiko ulio sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri REA yafuatayo, kama inataka kuutawanya umeme vijijini tutembee kwa asilimia inayofanana, tukisema Taifa tumepeleka umeme vijijini kwa 60% basi tuwe tumekaribiana, lakini kwa mfano leo Nanyumbu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi ya kutoa mchango wangu katika eneo hili la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kutoa ushauri au mchango wowote, nitumie fursa hii kuwashukuru sana viongozi wa nchi, hii hasa Jemedari wetu Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na viongozi hasa Waziri wa Maji, Naibu na watendaji wote wa Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kuizungumzia Nanyumbu kwa sababu tuna shida kubwa sana ya maji kwenye Wilaya yetu ya Nanyumbu. Nanyumbu tunaposema hatuna maji tafsiri yake ni kwamba hata maji ya kuokota ni shida. Kuna watu kijiografia tumekaa sehemu mbaya hata maji ya kuokota hayapatikani. Katika vijiji vya Nanyumbu tunapofika mwezi Juni maji yanakuwa ya shida sio ya bomba wala siyo hayo mnayosema maji bora sisi ya kuokota yanakuwa shida, tunapata sana shida ya maji hata ya kuokota, hata oga yetu inakuwa ya shida. Waziri ninapomwambia Nanyumbu kuna shida ajue kwamba hata maji ya kuoga ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa mkakati wake wa kuondoa shida ya maji katika mji wetu wa Mangaka ambapo ndipo Makao Makuu ya Wilaya ya Nanyumbu. Pale Mangaka tuliiomba Serikali itupatie maji kutoka chanzo kikubwa cha maji cha Mto Ruvuma, nashukuru Serikali ilifanya upembuzi yakinifu lakini baada kukamilisha ripoti Serikali ikabaini kwamba gharama ya kutoa maji kutoka Mto Ruvuma mpaka Mangaka ambapo ndiyo Makao Makuu ya Wilaya ni kubwa sana na ikaja na utaratibu wa kuyatoa maji kutoka Mbwinji kuleta Mangaka. Mimi kama Mbunge naishukuru sana Serikali kwa wazo hili zuri na naona jitihada ya Waziri namna ambavyo anakamilisha mchakato huu ili maji yaweze kupatikana pale Mangaka Makao Makuu ya Wilaya ya Nanyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina shida na hilo lakini ombi langu la kwanza. Naomba Mchakato huu uende kwa spidi nzuri Mheshimiwa Waziri, muda hautusubiri, 2020 ni kesho na mimi wananchi wangu walitaka maji. Natamani sana wakati wa kipindi changu maji hayo yaanze kufanyiwa kazi. Mheshimiwa Prof. Mbarawa nakuamini na nina mategemeo makubwa kwamba suala hili utalikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili kutoka Mbwinji kuja Nanyumbu sheria inasema kilomita 12 kutoka kwenye bomba kuu vijiji vyake vitapata maji. Naomba suala hili lizingatiwe katika kulishughulikia tatizo la maji pale Mangaka kwa sababu tuna vijiji vingi sana kutoka kule mpakani mwa Masasi na Nanyumbu mpaka kufika Mangaka. Kwa hiyo kama sheria itazingatiwa vijiji vingi vya Mangaka, vya Wilaya ya Nanyumbu vitakuwa vimepata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kushukuru hilo ambalo nina matumaini makubwa muda si mrefu mradi utaanza, nataka nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba kuna baadhi ya maeneo, ingawa tuna shida kubwa sana ya maji lakini tumetofautiana kutokana na eneo na eneo. Kuna Kata za Mnanje na Maratani, kata hizi zina shida kubwa sana ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Juni Mheshimiwa Waziri ukija Maratani hutaoga kwa sababu kuna shida kubwa sana ya maji, vyanzo vyote vya maji vinakauka. Pia ukija kwenye Kijiji cha Michiga ni kikubwa sana na kina watu wengi sana lakini hakina maji hasa inapofika mwezi Juni na kuendelea. Kwa hiyo, naomba sana katika mipango ya baadaye na mimi nitakaa na Waziri nitatoa mapendekezo ya maeneo ambayo tunatakiwa tupeleke miradi kwa haraka kabla ya vijiji vingine kutokana umuhimu na shida ya eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji haya yakifika Mangaka tulikuwa na matumaini makubwa sana ya kutoka Mangaka mpaka Masuguru ambako kulikuwa na chanzo cha Mto Ruvuma wangepata maji yale ya kwanza. Kwa mabadiliko haya vijiji hivi ni kama wamekumbwa na butwaa. Nitakaa na wewe tupendekeze namna ya kuweza kushughulika na vijiji hivi ili tuondoe tatizo kubwa la maji katika vijiji hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la kwanza twendeni tukachimbe mabwawa, tunayaacha maji yanakwenda mtoni na baharini. Bahati nzuri bado maji ya mvua yanapatikana lakini tunashindwa kuyadhibiti ili wananchi wetu waweze kupata haya maji. Kwa hiyo, nashauri sana Serikali iwekeze kwenye uchimbaji wa mabwawa aidha ya umwagiliaji lakini pia ya upatikanaji wa maji ya kunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Maliasili kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne, Mheshimiwa Maige yupo hapa aliahidi kusaidia maji kwenye Kijiji cha Masuguru na Kijiji cha Chinika aliahidi kutoa shilingi milioni 6. Mpaka leo nashindwa kukaa vizuri hapa Bungeni, wananchi wananikumbusha pesa ile, pesa ile ilitolewa ahadi na Serikali ya Awamu ya Nne. Mimi nataka iende pesa cash, Halmashauri itaongezea tutachimba visima, ahadi hii ni ya Serikali inatutia aibu sana. Serikali ya Awamu ya Nne aliahidi Mheshimiwa Ezekiel Maige na bahati nzuri nilikuwepo pale wakati ahadi inatolewa. Naomba sana unisaidie Mheshimiwa Waziri wa Maji kuikumbusha Wizara ya Maliasili wasisahau deni hilo wananchi wanakumbuka. Kama ninyi mmesahau lakini wananchi hawajasahau. Naomba sana ulitilie mkazo suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa ushauri, kutoka Mto Ruvuma mpaka walau Makao Makuu ya Tarafa ya Nanyumbu, Tarafa yenyewe ya Nanyumbu si mbali sana. Makao Makuu ya Wilaya ya Mangaka tunategemea maji kutoka Mbwinji lakini tuna uwezo pia wa kuanzisha mradi mdogo kutoka Mto Ruvuma mpaka kwenye Kijiji cha Nanyumbu ambako ni Tarafani pia tukaweza kusaidia kutoa maji kusaidia vijiji ambavyo vimezunguka ile Tarafa ya Nanyumbu. Tukifanya hivyo, nina hakika sana Wilaya ya Nanyumbu itakuwa imepata maji ya kutosha na hatimaye kero ya maji itakuwa haipo. Vijiji vingine sisi kama Wilaya tumejipanga namna ya kuweza kusaidia kwa sababu Halmashauri ina mtambo wa kuchimba visima virefu, basi tunaendelea kupunguza baadhi ya vijiji ambavyo vina shida ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, sisi Nanyumbu tuna pesa ya kuchimba mabwawa mawili, moja kwenye Kijiji cha Maratani na lingine kwenye Kijiji cha Namasogo. Taratibu zote kama Nanyumbu tumekamilisha ni ngazi ya Wizara inatuchelewesha na mvua zimeanza kuisha na ni vizuri mabwawa yakachimbwa kipindi ambacho mvua hainyeshi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa hebu nipe matumaini na wananchi wasikie, hizi pesa utazipeleka lini maana mkandarasi ameshapatikana, tunataka tu utoe go-ahead kazi ianze ili wananchi wa Kata ya Maratani na Namasogo wapate maji kama ambavyo Serikali ilikuwa imeahidi kushughulikia tatizo lao la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda kwenye ushauri sasa kwa sababu nimeweza kuyapunguza machache yanahusu Nanyumbu. Watu wengi sana wanaongelea hapa kuongeza nguvu ya Mfuko wa Maji. Mheshimiwa Waziri hayo unayokwama nayo hufanyi makusudi, huna fedha, lakini chanzo kikuu ambacho tumekiona hapa ni ile shilingi 50 ya kwanza, Wabunge wanapendekeza tuongeze, kuna ugumu gani Serikali kutusikiliza sisi Wabunge? Sisi tumechaguliwa msituone hivi, tumeaminika. Kama kuna hofu tutawaambia wananchi wetu kwamba hakuna kitu cha bure duniani ni lazima tufunge mikanda. Mimi naomba sana Serikali kubalini mawazo ya Wabunge, twendeni tuongeze shilingi 50 kwenye mafuta ili Mfuko wa Maji utune. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii bajeti iliyopita ya 2018/ 2019 mpaka leo una asilimia 51 tu ya pesa, tunajifunza nini hapo? Ni kwamba uwezo wetu wa kupambana na hii kitu bado ni mdogo lazima tuongeze nguvu. Nitashangaa sana ukija hapa Mheshimiwa Waziri usikubaliane na mawazo yetu, nitakushangaa kweli. Una muda, kaa na wenzako ambao mnakaa nao huko na ambao wana hofu, Wabunge ambao ni wawakilishi tumekubali tutakwenda kuwaeleza wananchi, sisi ndiyo tunakaa nao wale ninyi hofu ya nini? Serikali, sikieni hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vyanzo vingi mbali ya mafuta kuna simu. Mtu mmoja alisema hapa, hivi mtu akiona kwamba umenunua vocha ya Sh.1,000 akaona Sh.20 imeenda kwenye maji wananchi watakasirika, vingapi tunachangia wananchi wasikasirike? Maji ni shida kubwa kwa wananchi wetu tena wanyonge hawa ndiyo zaidi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa, muda wako umeisha. (Makofi)

MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri mawazo yangu yamesikika vizuri, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi ya kuweza kutoa mchango wangu wa mawazo katika bajeti hii. Awali ya yote nitoe shukrani zangu za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimwa John Pombe Magufuli kwa kuweza kutekeleza ahadi kubwa na muhimu kwa wananchi wangu wa Nanyumbu hasa Kata ya Mikangaula na Kijiji cha Mikangaula kwa sababu Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Kikwete alitoa ahadi ya kituo cha afya pale Mikangaula. Nami kama mwakilishi wao wananchi nilikuwa naendelea kuwasiliana na Serikali kuhakikisha kwamba ahadi inatimia. Hatimaye kwenye bajeti hii tumeshatengewa fedha kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuanza ujenzi huo wa kituo cha afya. Kwa niaba ya wananchi wale natoa shukrani za dhati kwa Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge nami nimeona niweze kuchangia eneo moja tu la kusisitiza namna ya kukusanya mapato ili Serikali yetu iweze kuwa na uwezo wa kuweza kutoa huduma kwa jamii. Eneo lenyewe ni namna ya kulinda vyanzo vyetu vya mapato. Hapa nakwenda kukiangalia chanzo cha ajira kwa sababu watumishi wanaoajiriwa na Serikali na kampuni za watu binafsi pia wanachangia katika kulipa kodi ya Serikali. Sasa ni vizuri Serikali ikawa makini kuhakikisha kwamba hao watu ambao wanaajiriwa wanalindwa ili wasipotee kwa sababu wakipotea Serikali inakuwa imepoteza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kutoa mfano mdogo tu ambao naomba Mheshimiwa Waziri auzingatie. Wakati natunga Sheria ya TASAC hapa, Sheria ile ilikwenda kuwaondoa watu wanaitwa watu wa tallying. Watu wa tallying ni kama mashuhuda wa mwenye mzigo, mwenye mzigo akiwa nje akileta mzigo wake hapa anataka watu anaowaamini yeye wauthibitishe kama mzigo kabla haujapokelewa na bandari kama umekuja kama alivyoagiza yeye. Pia kama kuna mzigo unaondoka Tanzania kwenda nje labda majani ya chai, anataka mtu anayemwamini yeye akaungalie mzigo kama ni kweli ndiyo unaopakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tumekwenda kuwaondoa mashuhuda hawa ambao watu wa nje wanapenda kuwaamini. Sasa hii kitu ina athari nyingi, kwanza tunaondoa ajira lakini pili tunakwenda kupoteza kodi ambayo Serikali ingeweza kupata, tatu Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ilikuwa imeahidi kuhakikisha kwamba tunaongeza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nishauri Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba suala hili la TASAC, kitendo cha kuwaondoa watu wa tallying tunakwenda kufanya makosa makubwa ambayo yataathiri maeneo mengi na makubwa. Kwa hiyo naomba atakapokuja hapa aangalie uwezekano wa kuleta mapendekezo ya kubadilisha sheria ili itakapofika mwezi Julai kama ambavyo wamewaahidi wasije wakawaondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakwenda kuangalia kule jimboni kwangu na kutoa ushauri mchache, naanza kwenye suala la umeme, umeme Nanyumbu ni shida; Nanyumbu ina umeme usiozidi asilimia 30 ya vijiji vyote ambavyo vina umeme. Nanyumbu tulipata umeme kwa mpango maalum wa Serikali laini REA I Nanyumbu haikupatikana, REA II haikupatikana, REA III tukapata vijiji 13. Kwa hiyo, nashauri Serikali inapoona kuna wilaya au eneo ambalo limekosa umeme kwa kiasi kikubwa basi tunapokwenda kugawa huu umeme watu kama hawa wanatakiwa wapate zaidi kuliko wale wengine. Kwa sababu kuna watu wana asilimia 90 ya vijiji vyao, kuna watu wana asilimia 80 lakini Nanyumbu ina chini ya asilimia 30. Kwa hiyo, nilitegemea bajeti iliyopita tungepata vijiji vingi, kwa hiyo, leo nakwenda kuunga mkono hii bajeti lakini nataka nione kwamba vijiji vyangu vingi vinapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano ukija Makao Makuu ya Wilaya ya Nanyumbu pale Mangaka ukitembea mita 20 nje ya barabara hakuna umeme. Kuna Kitongoji kimoja kinaitwa Mchangani, kama Mbunge naona aibu kupita kule kwa sababu ni mjini pale pale hakuna umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba hawa watu wanapoanza kushuhulikia haya mambo wahakikishe kwamba maeneo makubwa kama Makao Makuu ya Wilaya tuhakikishe umeme unapatikana. Kuna wilaya zina umeme wa kutosha kwa nini Nanyumbu iwe hivyo. Kwa hiyo, napendekeza TANESCO wapewe uwezo wa kuweza kukabiliana na hili eneo langu la Nanyumbu ili wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu wapate umeme, wasiwe watu wa kulalamika kwa sababu sasa wanajisikia vibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maji yanayotumika pale Mangaka yanatoka kwenye Kijiji kimoja kinaitwa Mara, ni kilomita kama nane kutoka Makao Makuu ya Wilaya. Yale maji tunatumia jenereta laini umeme upo kilomita nane, sasa jenereta zinaharibika wananchi wanakosa maji lakini hata hivyo gharama za uendeshaji ni kubwa, maji yanauzwa kwa bei kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kwenye bajeti hii umeme upelekwe haraka pale kwenye chanzo cha maji ili wananchi waweze kupata maji kwa bei nafuu lakini pia kwa uhakika. Umeme uliotoka Mangaka kuelekea Tunduru hapo katikati pana vijiji vingi sana lakini umeme umeteremka Kijiji cha Mnazi Mmoja pale Michiga peke yake, lakini vijiji vyote vya njiani vimekosa umeme laini kubwa zipo lakini umeme umekosekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri na kuomba Serikali kabla hatujaanza kutoa vijiji vingine tuhakikishe vijiji hivi ambavyo vinapitiwa na laini kubwa vinapata umeme. Kwa mfano Likokola ni Makao Makuu ya Kata hakuna umeme, pana zahanati; Lumesule Makao Makuu ya Kata hakuna umeme lakini pana zahanati. Kwa hiyo, naomba tuvipatie umeme vijiji hivi ili wananchi hawa nao wapate umeme kwa sababu umeme ndiyo maendeleo bila umeme kimsingi huwezi kuwa na maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nilichangie ni TARURA, TARURA hao ukiwachunguza matatizo yao wana fedha ndogo sana. Wilaya yangu haipati zaidi ya milioni 800 ukilinganisha na ukubwa wa barabara ambazo zipo Nanyumbu hii kitu hawawezi kukabiliana nayo. Kwa hiyo, wananchi wanakuja kuilaumu Serikali, wananchi wanakuja kukilaumu hiki chombo cha TARURA hata sometimes Madiwani kwa sababu bado wananchi hawajaelewa vizuri huu mtenganiko. Kwa hiyo, Madiwani wanapata lawama ambayo siyo yao, sasa naomba sana tuongeze fedha kwa hizi barabara za vijijini lakini pia hata hiyo fedha ndogo ambayo tunawapa kuna tabia ambayo ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watendaji hawa wa TARURA wa Ofisi Kuu Mkao Makuu TARURA wanatenga labda milioni 800 Nanyumbu, lakini baadaye wakati Nanyumbu imeshingia mikataba ya kutengeneza ile barabara TARURA wanawaandikia barua kwamba sasa mtatumia milioni 600. Sasa hawa wameshaingia mkataba, kwa hiyo tunasababisha mgogoro kati ya TARURA na wakandarasi, tunasababisha mgogoro kati ya TARURA na Madiwani na wananchi hatimaye Serikali yote inakuwa imepata lawama ambazo siyo za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba sana Serikali tunapotenga hata hicho kidogo ambacho tumekisema kiende, kwa sababu unaposema kisiende wakati wameingia mkataba ni hatara sana. Tunaweza kusababisha hata kushtakiwa na hao wakandarasi, nashukuru sana wakandara wanakuwa wastaarabu lakini kimsingi wanaweza wakatuchoko. Hilo suala naomba sana Serikali iliangalie kwa makini ili tusije tukasababisha migogoro ambayo kimsingi tunaweza tukaiepuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo sikutaka niongee mengi ila nirudi tena kwenye swali langu la mwisho kabisa la umeme. Nanyumbu kama nilivyosema tupo chini sana, ninaunga mkono bajeti hii nihakikishe kwamba Nanyumbu kwenye umeme tutakuwa tumepata vijiji vingi kwa sababu ya nature ya tulikotoka Tulisahauliwa, kwa hiyo tukipendelewa ni sahihi siyo Nanyumbu peke yake, wale wote walioachwa nyuma wakipiwa mwingi awamu hii ni halali yao kwa sababu kuna watu wana vijiji vingi sana. Hilo suala naomba sana Serikali katika awamu hii, na naunga mkono hoja hapa ya bajeti kwa matumaini hayo Mheshimiwa Dkt. Mpango. Nahakikisha kwamba tunaunga mkono bajeti lakini ikatimize haya ambayo wananchi wanategemea wayaone. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana muda wangu nimeutumia vizuri naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, awali ya yote niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara, hakika wanatenda kazi, hatuna shaka nao katika utendaji wao wa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ya Wizara hii tunafahamu kwamba ni pesa, lakini mimi naiomba sana Serikali, hapa naiambia moja kwa moja Serikali, hizi pesa ambazo tumezitenga kwa ajili ya Wizara hii naiomba Serikali ihakikishe kwamba inazipeleka kadri zinavyopatikana na ikiwezekana zipatikane kwa asilimia mia moja, kwa sababu kama wanavyosema watu maji ni uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa sababu katika bajeti hii, kabla ya hapo nilikaa na Mheshimiwa Waziri nikamueleza tatizo kubwa la bwawa letu kule katika Kijiji cha Namasogo na tatizo la mfumo wa maji taka pale Mangaka mjini. Nashukuru katika bajeti hii nimetengewa shilingi milioni 400 katika Bwawa la Namasogo, lakini pia shilingi milioni 500 kwa ajili ya mfumo wa maji taka pale mjini Mangaka kwa kweli nawashukuru sana kwa hiki, kidogo ambacho tumeanza nacho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Katika bajeti hii pia tumetengewa pesa zaidi ya shilingi milioni 1300 kwa ajili ya maji vijijini. Basi hizi pesa nalihakikishia Bunge lako tukufu tutakwenda kuzisimamia, mimi pamoja na Madiwani wenzangu kule tukiongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri kuhakikisha kwamba lengo la Serikali linatimia. Kwa sababu kama Diwani nina jukumu la kusimamia pesa hizi ili zifanye kazi tarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa Wilaya ambazo zinashida kubwa sana ya maji katika nchi hii ni pamoja na Nanyumbu. Kwa hiyo, ninaomba sana Serikali katika bajeti zingine iangalie wilaya gani zina tatizo kubwa katika mgawanyo wa hizi pesa ili tuweze kufanana katika kutatua tatizo kubwa la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Ruvuma mpaka Mjini Mangaka. Serikali ilikuwa imeshandaa utaratibu wa kuyatoa maji kutoka Mto Ruvuma na kufikisha katika makao makuu ya Wilaya pale mjini Mangaka. Hatua tuliyokuwa nayo ni ya usanifu wa kina na kuandaa makabrasha kwa ajili ya kutangaza zabuni. Sasa niiombe Serikali, kwanza speed ya upembuzi yakinifu iwe kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda hautusubiri lakini wananchi wanatusubiri. Kwa hiyo nashauri sana hawa watu tuliowapa hili jukumu wafanye kazi kwa speed ili wananchi waone matokeo ya sisi kuwa viongozi wao katika awamu hii ya tano.

Kwa hiyo nashauri sana Wizara isituangushe katika utendaji wa kazi ili maji kutoka Mto Ruvuma yafike pale mjini Mangaka. Lakini nilishaomba na tena naomba yale maji upembuzi yakinifu uelekee hadi Lumesule kupitia Michiga na Likokona. Vilevile tufike pia Nagomba, Mikangaula, na Mpakani mwa Wilaya yetu na Masasi pale Namatumbusi. Tukifikisha maeneo hayo nia uhakika kwamba tumesaidia eneo kubwa la Wilaya ya Nanyumbu kupambana na shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya kwa sababu muda wangu ni mdogo sana, basi naunga mkono hoja, nashukuru, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kupongeza Wizara na hasa utendaji uliotukuka wa Waziri na Naibu wake.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono kwa dhati kabisa ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme kule Rufiji. Ni wazi kuwa umeme wa maji utashusha gharama za umeme hivyo wananchi wengi kumudu gharama, lakini pia uwekezaji utakuwa rahisi kumudu ushindani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Nanyumbu ilipata umeme kwa mara ya kwanza mwaka 2013 kwa mpango maalum wa Serikali. Vijiji vilivyopatiwa kipindi hicho ni 23 kati ya 93 kwa bahati mbaya sana REA awamu ya kwanza nay a pili Nanyumbu ilikosa. REA awamu ya tatu Nanyumbu ilipatiwa Vijiji 13 tu. Niliomba nyongeza ya vijiji 17 ili kufanya vijiji 30, ombi ambalo Waziri alikubali kwenye mkutano wa hadhara katika uzinduzi wa REA awamu ya tatu pale Michiga.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tunatarajia kufikia asilimia 84 ya vijiji vitakavyopata umeme ifikapo 2020, naomba kufanyika upendeleo wa maeneo yaliyobaki nyuma kama Wilaya ya Nanyumbu. Vijiji vilivyopo kati ya Mangaka na Lumesule ambapo HT imepita na vijiji hivyo kukosa umeme, vipewe kipaumbele katika utekelezaji wa REA III.

Mheshimiwa Spika, Mjini Mangaka, Makao Makuu ya Wilaya ya Nanyumbu maeneo mengi hayana umeme, hasa Mtaa wa Mchangani, nashauri eneo hili lifanyiwe kazi haraka. Mji wa Mangaka unapata maji toka kwenye bwawa la Kijiji cha Mara ambapo maji yanasukumwa kwa kutumia jenereta ambapo linaharibika mara kwa mara pia gharama za uendeshaji huwa juu.

Mheshimiwa Spika, naomba umeme uende katika eneo hili. Endapo tutapeleka umeme eneo hili tutakuwa tumevipatia vijiji vya njiani umeme ambavyo ni Matimbeni KCU na Sengenya KCU.

Mheshimiwa Spika, kasi ya mkandarasi anayefanya kazi Mkoani Mtwara ni ndogo, hadi sasa ni kijiji kimoja tu ndio kimewashwa na vijiji vingine ni hatua ya kusimika nguzo.

Mheshimiwa Spika, nashauri katika kutengeneza mpango wa kupeleka umeme eneo fulani REA izingatie ushauri wa wataalam wa eneo husika, kwani nimeona makosa ambayo kama aliyepanga angekuwa ni mwenyeji baadhi yake yasingetokea.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. WILLIAM D. NKURUA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Natoa pongezi kwa Serikali na Wizara kwa kazi nzuri wanazozifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda si rafiki, nakwenda moja kwa moja kwenye Jimbo langu la Nanyumbu. Hapa naanza na watu wa ujenzi; napenda niwakumbushe kwamba Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alitoa ahadi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami toka Nangomba mpaka Nanyumbu. Barabara hii ni barabara inayoelekea nchi jirani ya Msumbiji, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Tanzania. Kwa hiyo naomba Serikali katika vipaumbele vyake iiweke barabara ya kutoka Nagomba hadi Nanyumbu kwa sababu wananchi wana imani sana na ahadi ile na ukizingatia kwamba viongozi hawa wanakuwa wakweli. Kwa hiyo, naomba Serikali iiweke katika mpango wake ujenzi wa barabara kutoka Nangomba hadi Nanyumbu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Sekta ya Mawasiliano, naupongeza sana Mfuko kwa kazi kubwa inayofanya na kwenye Wilaya yangu ya Nanyumbu nataka niwape maeneo muhimu ambayo kwenye bajeti hii tuyazingatie. Kwanza kabisa nataka Kata yangu ya Napacho; kata hii ina shida kubwa ya mawasiliano, hasa kwenye Vijiji vya Mpombe, Ndekela, Mburusa, Napacho, Kazamoyo na Chimika, hawa watu mawasiliano ni magumu sana, naomba eneo hili tutafute eneo tuweke mnara, tukiweka mnara mmoja katika eneo hili tutahakikisha kwamba wananchi watapata mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Kata ya Likokona; kata hii pia haina mawasiliano, hata makao makuu ya kata mawasiliano ni magumu sana. Kwa hiyo naomba tutafute namna ya kuhakikisha kwamba Likokona na Vijiji vyake vya Msinyasi, Namaka na vitongoji vyake vipate mawasiliano ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naongeza Kata ya Mkonona; kata hii ina Kijiji cha Mbangara Mbuyuni na Kitongoji chake cha Wanika, mawasiliano hayapatikani kabisa. Kwa hiyo naomba Serikali itupatie mnara kwenye kata hii ili wananchi wa kata hii nao wapate mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho kwa mawasiliano ni Kata ya Maratani katika Wilaya ya Nanyumbu. Kata hii pia ina Vijiji vya Maratani, Malema na Mchangani B, havina mawasiliano kabisa. Naomba tupatiwe mnara katika maeneo hayo kutokana na viwango vyao vya kutambua wapi tuweke mnara ili vijiji hivi nilivyovitaja vipate mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri; minara hii itakayojengwa ijengwe kwa viwango ambavyo tutapeleka mawasiliano kama ilivyokusudiwa kwa sababu kuna baadhi ya vijiji minara imejengwa lakini haifanyi kazi ilivyokusudiwa. Kwa mfano, ukienda kwenye Kata ya Sengenya, Kijiji cha Sengenya, kuna mnara pale lakini mnara ule hata pale kijijini haufanyi kazi vizuri. Kwa hiyo naomba Serikali tunapoweka hii minara tuhakikishe kwamba inafanya kazi tuliyokusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Kata ya Mkonona, Kijiji cha Marumba, kuna mnara wa TTCL pale, lakini mnara ule haufiki hata kilometa tano, Vitongoji vyake vya Namaromba network haipatikani kule. Kwa hiyo naomba tutakapokwenda kupeleka minara hii, vijiji hivi na vitongoji vyake viweze kupata network na wananchi wetu waweze kupata mawasiliano kama tulivyokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda si rafiki, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)