Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Susan Limbweni Kiwanga (1 total)

MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Mheshimiwa Waziri Mkuu, utaratibu wa kibajeti unaanzia kwenye Serikali za vijiji mpaka inamalizikia Bungeni ndio tunapitisha bajeti ya Serikali. Lakini mpaka hapa ninapoongea kuanzia mwaka 2014 kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kuna vijiji vitatu vilisimamishwa na Ofisi ya TAMISEMI visifanye uchaguzi ingawaje vilishatangazwa kuwa vijiji. Vijiji hivyo viko katika kata ya Mofu ambapo ni Miomboni, lakini Kata ya Namohala ni Idandu na Chiwachiwa. Lakini kwa maelezo ya Serikali kwamba yale maeneo ni ya uwekezaji kwa hiyo hakuna uchaguzi wa vijiji utakaofanyika.
Je, Waziri Mkuu nini kauli ya Serikali kuhusu hatma ya vijiji hivyo na wananchi katika hilo Jimbo la Mlimba na kata na vijiji nilivyovitaja? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Susan Kiwanga kwa eneo lile la kisera zaidi badala ya kujikita kwenye ngazi za vijiji na hasa alipokuja kutamka kwamba kuna mwelekeo wa kibajeti kwenye ngazi za vijiji mpaka Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mchakato wa bajeti huanza kwenye ngazi za vijiji inaenda kwenye Kata, Wilaya na hatimaye Mkoa na baadaye unakuja kwenye Wizara. Hii inatoa nafasi kwa kila eneo kutengeneza mpango wake wa matumizi ya kifedha ili kuboresha masuala mbalimbali yakiwemo na mambo ya maendeleo. Na kama lipo tatizo ndani ya Halmashauri ya Wilaya linalogusa vijiji na wamekosa nafasi ya kuweka bajeti zao ngazi ya juu inawajibika kuweka bajeti ya maeneo hayo ambayo hayajapewa uongozi unaosimamia utengenezaji wa bajeti kwenye eneo hilo ili na wao waweze kupata huduma.
Mheshimiwa Spika, na kwa hiyo basi kama vijiji vile vitatu havijapata nafasi ya kuunda uongozi utakaoweka bajeti ya maendeleo yao ngazi ya kata ambako kuna Diwani ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Kata ndiye atakayewajibika kuviingiza vijiji vile kuvitengenezea bajeti kwenye kata yake na diwani atabeba kupeleka kwenye Halmashauri ya Wilaya na atalazimika kuviingiza kwenye mpango wa bajeti wa Halmashauri ya Wilaya vijiji hivyo ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma. Hata kama vijiji hivyo havijapewa nafasi kwa sababu tu eneo hilo ni la uwekezaji. Bado Serikali inatambua kuna wananchi pale na ni lazima wahudumiwe kwa hiyo bajeti lazima pia ioneshe kwamba wananchi wale watahudumiwa kadri wanavyokwenda mpaka hapo jambo hilo litakapopata utatuzi wake.
Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mchakato wa kibajeti unahusisha Watanzania wote, hata kama kwenye maeneo hayo kuna upungufu wa viongozi waliopo wanayo dhamana ya kutengeneza bajeti. Kwa hiyo basi, Wizara ya TAMISEMI na bajeti yao yote ya nchi nzima lazima vijiji hivyo viweze kushughulikiwa.
Mheshimiwa Spika, lakini suala la mgogoro wa vijiji hivyo sasa, na Waziri mwenye dhamana yuko hapa atakuwa ameshachukua jambo hilo na atawajibika sasa kufuatilia kule Ifakara na aweze kukupa jibu katika kipindi hiki cha Bunge ili utakaporudi nyumbani uwe na majibu ya hatma ya vijiji hivyo na uwekezaji uliopo maeneo hayo. (Makofi)