Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Abdulaziz Mohamed Abood (4 total)

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Kwanza nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali yangu ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri inayoendelea kuifanya. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti ya mwaka 2016/2017 niliwahi kumwambia Mheshimiwa Waziri kuhusu matatizo ya hospitali ya Mkoa wa Morogoro, kuhusu x-ray machine, majokofu ya kuhifadhia maiti na upungufu wa madaktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila iwapo nisipomshukuru Waziri na Naibu Waziri. Walishughulikia tatizo ya x-ray machine, walitutumia Wataalam ambao machine yetu ilikuwa ni analogue wakaibadilisha kuwa digital na sasa inahudumia wagonjwa 50 mpaka 70 kwa siku. Pia tumeweza kuunganishwa katika mfumo wa tele-medicine ambao wanapata ushauri zaidi kwa Madaktari Bingwa.

Kuhusu majokofu tunamshukuru Mheshimiwa Waziri ametupatia na sasa katika wiki hii yanaanza kutolewa ya zamani na kuwekwa mapya katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Upungufu wa madaktari tunashukuru Mheshimiwa Waziri umetutimizia kiasi kikubwa ila tuna tatizo bado moja kubwa la specialist wa ENT ambaye hatuna hata mmoja.

Pili, tuna tatizo vilevile la wafamasia ambao walitakiwa wawe 14 lakini tunae mmoja tu msaidizi. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri katika hilo naamini kwa kazi unazozifanya na Naibu Waziri kwa speed ya Awamu ya Tano mtatumalizia kero hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kero nyingine ni wodi ya wazazi katika hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Hospitali ya Mkoa inapokea wazazi 40 kwa wastani kwa siku na wodi inaweza kupokea wagonjwa 20 mpaka 25 tu kwa siku. Kwa hiyo, tungeomba Mheshimiwa Waziri atuongezee wodi nyingine katika bajeti yake ili tuweze kutimiza mahitaji ya wazazi katika wodi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kero nyingine tuliyonayo Morogoro ni ambulance. Tunayo ambulance moja tu na wagonjwa wanakuwa ni wengi mno kiasi ambacho wengine wanaandikiwa rufaa ya kwenda Muhimbili, ambulance moja inashindwa kufanya kazi yake. Kwa hiyo, tunakuomba Mheshimiwa Waziri uliangalie hilo na nitakupa ushirikiano ili tuweze kupata ambulance mpya nyingine kwa ajili ya hospitali ya Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo lingine la gharama za wanaovunjika viungo kwa maana ya wanaovunjika mifupa kwenye ajali na matatizo mengine. Gharama zile katika Hospitali ya Mkoa ambao hawana bima ya afya ni kubwa mno kuanzia shilingi 500,000 mpaka shilingi 700,000, lakini ukiuliza unaambiwa kwa sababu ya gharama ya vyuma.

Kwa hiyo, tunakuomba Mheshimiwa Waziri uliangalie hilo kwa sababu gharama hizi kwa watu wa hali ya chini wanashindwa kumudu, tungeomba mtufikirie juu ya hili ili tuweze kupata vyuma na vifaa vingine kwa ajili ya kuweza kupunguza gharama hizo ili wananchi waweze kugharamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya ya kutekeleza ahadi za maji katika Jimbo letu la Morogoro Mjini. Tunamshukuru alituahidi atatupa mradi wa maji na kweli sasa tumepata mradi wa maji, naishukuru sana Serikali, ila ninachoomba kwa Mheshimiwa Waziri tuharakishe huu mradi wa maji ambao tulimepewa na Wafaransa ili kuondoa kero hii ya maji, na hasa wakazi wa Morogoro wanazidi kuongezeka wakiwemo Wabunge wengine humu wakihamia Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna eneo la uwekezaji ambalo linahitaji maji mengi kwa ajili ya kuwekeza kwenye viwanda na wawekezaji wengi wakija kitu cha kwanza wanachouliza ni maji. Kwa hiyo, tunaomba Wizara iharakishe kazi hii ya mradi huu wa maji ili tuweze kupata maji kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Morogoro bado kuna tatizo la maji. Huu mradi ni mradi wa muda mrefu lakini sasa hivi bado tuna tatizo la maji. Bwawa la Mindu limejaa lakini miundombinu inayokwenda na kusambaza katika maneo mbalimbali ya Morogoro bado ni tatizo. Kwa hiyo, naomba Wizara iliangalie hilo ili kuongezea bajeti upande wa Morogoro kwa ajili ya kuweza kutengeneza miundombinu mipya ambapo maeneo mengi kuna miundombinu chakavu; na hasa maeneo ya Kihonda, Tungi, Lukobe, Mkundi na Kiyegeya. Cha kushangaza zaidi wananchi wa Mindu ambao wanalilinda lile bwawa la maji kwao hakuna maji wala miundombinu ya maji, kwa hiyo, naomba Wizara waliangalie hilo ili tuweze kuondoa kero hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi ya World Bank ambayo wananchi wamechangia. Sasa kuna tatizo ambalo Mheshimiwa Waziri naomba hili mlifanyie kazi, kuna kata mbili kata ya Bigwa na Kingolowila, kuna mitaa minne ambayo wananchi wamechangia mradi huo lakini mradi huo unataka kuchukuliwa na kupewa MORUWASA. Ila wananchi sasa wanadai wanasema miradi wameshachangia wao wanahitaji wao wenyewe waendeshe hiyo miradi ya maji kwa kutumia vikundi vyao vya ushirika. Tatizo linalokuja ni kusema kuwa sheria hairuhusu. Mimi nadhani wakati wananchi walipokuwa wakichangia ilitakiwa waambiwe kwamba mradi huu hamtoweza kuendesha wenyewe. Sasa hivi kuna mgogoro mkubwa sana katika maeneo haya. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri, elimu ya kutosha inatakiwa kwa wananchi ili kuepukana na tatizo hili la kudai kuendesha mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu wamepewa MORUWASA na bei wanayowapangia sasa hivi ni kubwa, kwa hiyo, hawakubaliani nao na mradi umesimama na wananchi bado wanaendelea kukosa maji. Tunaomba hili tatizo lifanyiwe kazi ili tuweze kulimaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo lingine kubwa bado linaendelea na hasa tunategemea kupata mradi mkubwa wa maji, Mjini Morogoro. Tatizo ni bili za maji wananchi wanalipa maji ambayo kwa mwezi mzima au miwili hajapata lakini anapata bili ametumia maji, ni kutokana na mita zenyewe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti ya mwaka 2021/2022. Natumia nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya. Nawapongeza Mawaziri wote, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu, kwa kazi nzuri mnayoendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake kwa bajeti nzuri sana. Naunga mkono bajeti kwa asilimia 101. Ila hii moja naitoa kwa sababu katika kusoma bajeti yake, hakuitaja Simba, kaitaja Yanga peke yake. Kwa hiyo naibakisha asilimia 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nijikite kwenye Sera ya Viwanda. Tanzania tupo kwenye Sera ya Viwanda. Ili tuwe na viwanda vingi ambavyo vinamilikiwa na wazawa wenyewe, lazima tuwe na investment banks. Tanzania hatuna investment banks, tunayo moja tu ambayo ina mtaji mdogo. Lazima tuwe na investment banks zenye mitaji mikubwa ambazo zinaweza zikakopesha na wananchi wakaweza kufungua viwanda vikubwa vitakavyotoa ajira nyingi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukichukulia kwa mfano TIB, tuna benki moja tu Tanzania na mtaji wake ni mdogo. Ukichukua majirani zetu Wakenya, wana investment banks karibu kumi na riba yao iko chini, 4%. Sisi hapa Tanzania riba yetu ni kuanzia asilimia 12 mpaka 18. Kwa hiyo ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba tujitahidi; na hasa hizi pension funds zote tungezifanya pia investment banks ili ziweze kutoa mikopo ya muda mrefu kwa wawekezaji wazawa wa Tanzania na mikopo mikubwa ili kuwekeza katika viwanda na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye viwanda vya kilimo bado tuko nyuma sana, tunahitaji lazima tuwekeze kwenye viwanda hivi. Viwanda hivi vinategemea sana wakulima. Sasa jinsi ya kuwakopesha wakulima nayo vilevile Serikali iangalie. Kwa sababu ukitazama wakulima wa nchi mbalimbali duniani, huwa wanakopeshwa kwa riba ndogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukichukua Malaysia ambao ni wakulima wakubwa wa mawese; minimum mkulima anakopeshwa shilingi bilioni tano kwa ajili ya kilimo cha mawese kwa miaka kumi. Hapa Tanzania agro-processing inahitaji tuwe na sera ya muda mrefu, siyo ya mwaka kwa mwaka, ili wakulima wajitayarishe; na wenye viwanda wanaokopa wawe na sera ya muda mrefu ya kuweza kuzalisha mazao haya, kama ni mafuta ya kula, kama ni nini, ili kama anakopa anaweza akarudisha mkopo wake kwa muda wa miaka kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala lilishawahi kutokea mwaka 2004. Wakulima walilima sana alizeti, baada ya kodi ya mafuta kupanda. Baada ya mwaka mmoja kodi ikaondolewa, wakulima wakazima. Kwa hiyo, mimi naomba sera iwe ya muda mrefu, siyo ya mwaka kwa mwaka ili viwanda hivi vya agro-processing viweze kujipanga kwenye kilimo kwa muda mrefu na wakikopa wajue kabisa kwa miaka kumi, sera haitabadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, linguine ni kuhusu pesa za wahisani zinazokwenda kwenye miradi mikubwa. Pesa hizi naishauri Wizara ya Fedha kwa kumtumia Msajili wa Hazina, wafuatilie. Kwa mfano, Morogoro, tumepata Euro milioni 70 kwa ajili ya mradi wa maji, ambayo ni sawasawa na shilingi bilioni 180, lakini Wizara ya Maji mpaka leo hatujui kama hizo pesa zimefika na Morogoro mradi hakuna. Sasa tunataka tujue, hizo pesa ziko wapi ili mradi wa maji uanze? Sasa Hazina nayo itusaidie kutupa majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri amekuja kule, ametumbua tumbua, hatujui pesa ziko wapi? Kwa hiyo, naishauri Serikali kwa kumtumia Msajili wa Hazina, miradi mikubwa kama hii ingekuwa inafuatiliwa ili tuwe tunapata majibu ya haraka kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme tu,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Naibu Spika, naona muda wangu umekwisha. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa Abdul-Aziz Abood.

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii kuchangia Hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza nichukue fursa hii ya kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri Mkuu na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi nimesikia wakizungumzia kuhusu kilimo na ajira. Tatizo kubwa ambalo lipo sasa hivi ni vijana wengi kukosa ajira, lakini njia fupi na njia nyepesi duniani kote kuondoa uhaba wa ajira ni kilimo na hasa kilimo cha umwagiliaji. Tanzania tuna kila aina ya uwezo wa kufanya kilimo cha umwagiliaji. Tuna maziwa, tuna mito, tunaweza tukajenga mabwawa makubwa ya kuweza kukinga maji ya mvua na kufanya kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nijikite kwenye kilimo kimoja tu cha mpunga. Kilimo cha mpunga Tanzania tunaweza kuwa wazalishaji wakubwa Kusini mwa Afrika na Bara zima, kama tutaweza kutumia ardhi yetu vizuri katika kilimo hiki cha mpunga na hasa kilimo cha umwagiliaji. Kwa mfano, Morogoro tuna eneo linalofaa kwa umwagiliaji hekta 1,510,339 wakati eneo hilo sasa hivi linatumika hekta 40,558. Kwa hiyo, ninaishauri Serikali tujaribu sana kujikita upande huo na ajira kubwa itatoka kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nirudi Jimboni. Morogoro tuna tatizo kubwa la maji, tunao mradi wa maji wa AFD wa Shilingi Bilioni 180 lakini mpaka leo hii bado ni hadithi tu, kila siku tunasaini, tunatangaza, tunafanya hivi, tunafanya hivi. Ninaiomba Serikali itusaidie ili mradi huu uweze kutekelezwa usaidie Manispaa ya Morogoro na Morogoro unajua ni sehemu ya uwekezaji mkubwa unahitaji maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wawekezaji wanakuja kitu cha kwanza wanauliza maji yapo? na sisi tuna upungufu mkubwa sana wa maji na hasa katika Mji wa Morogoro maeneo mengi sana yamepata miradi midogomidogo ambayo Serikali imetoa pesa zake lakini imetoa pesa kutengeneza tenki, kupeleka mabomba lakini mabomba ya kusambaza kwa wananchi haikutoa pesa. Kwa hiyo, ninaomba Serikali itufikirie katika Bajeti hii 2022/2023 kutupatia pesa katika miradi hii ili iweze kupunguza kero ya maji katika Manispaa ya Morogoro, kusambamba mabomba kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kero ingine katika Halmashauri ya Morogoro tuna stendi mpya ambayo kijiografia ya Manispaa ya Morogoro iko mbali na wananchi. Kwa hiyo, wananchi wana safari ndefu ya kwenda kupanda basi kule wa mabasi ya daladala haya. Tuna stendi ya zamani iko Mjini Manispaa ya Morogoro, lakini nashangaa stendi ile haitumiki lakini imeamuliwa yale mabasi yapaki barabarani palepale karibu na stendi wakati Halmashauri inapoteza Shilingi Milioni 32 kwa mwezi. Tungeruhusu yale mabasi yaingie pale ingeweza kulipa hata deni ya stendi mpya. Kwa hiyo, mimi ninaiomba Serikali irudishe stendi ya zamani ili iendelee kutumika, wananchi wa Morogoro wapate huduma kwa sababu eneo kubwa la Morogoro linatumika ni stendi ya Morogoro Manispaa ya Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika sekta ya Afya tuna Hospitali ya Wilaya. Hii hospitali ya Wilaya tumepewa Shilingi Milioni 500 tu ambazo zimefika kujenga OPD na Maabara, hakuna maeneo ya kulaza wagonjwa. Kwa hiyo, tunaomba Serikali Mradi huu tuumalize kwa sababu huu mradi una miaka saba sasa, tunaomba Serikali itumalizie mradi huu ili tupate na wodi za wagonjwa katika Hospitali hii ya Wilaya ya Morogoro. Katika bajeti tulitengewa Milioni 500 hazitoshi, tunaomba tuzidishiwe ili tumalize, kwa sababu Hospitali ya Mkoa wa Morogoro imeelemewa. Kwa hiyo, tunaomba na Hospitali ya Mkoa wa Morogoro nayo iweze kupata upanuzi wa majengo yake ili nayo iweze kupokea wagonjwa wengi zaidi, kwa sababu Morogoro ni katikati ya Miji yote, wagonjwa ni wengi, ajali zinatokea nyingi zinahitaji Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ya Rufaa ipanuliwe iwekwe majengo mengine yaongezwe ili iweze kutoka huduma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kutoa ushauri kwa Serikali kwa sababu sisi Wabunge tuna wasaidizi. Wasaidizi wenyewe katika Majimbo yetu ni Madiwani, Madiwani wasaidi wao ni Wenyeviti. Kwa hiyo, mimi ninaishauri Serikali hali ya Madiwani na Wenyeviti na hasa Madiwani hali zao katika kipato ni kidogo sana. Kwa hiyo, ninaishauri Serikali tuwaongezee kidogo ili wafanye kazi vizuri, hata sisi Wabunge tunapokwenda kwenye Kata zao tunakuta kidogo kumechangamka na wameweza kuzungukia Kata zao. Kwa hiyo, maslahi yao tuyaboresha kidogo Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa, tuwape posho za kuweza kujikimu katika kutumikia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono. (Makofi)