Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Issa Ali Abbas Mangungu (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kupata nafasi hii kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha leo kusimama hapa nikiwa Mbunge wa Jimbo la Mbagala. Pili, nimpongeze na niwapongeze wote ambao wameshinda katika Uchaguzi Mkuu huu akiwemo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluh Hassan, Mawaziri na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchangia moja kwa moja hotuba ya Waziri Mkuu katika eneo la ajira. Jimbo langu la Mbagala lina viwanda ambavyo vinachangia pato la Taifa, vinachangia kodi lakini kumekuwa na malalamiko na manung’uniko mengi ya wafanyakazi katika viwanda hivyo. Waajiri wamekuwa wananyanyasa wafanyakazi, wanawatumikisha zaidi ya miaka sita mpaka miaka nane hawawapi mikataba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru tangu Serikali ya Awamu ya Tano ilivyoingia nimekuwa nikilifuatilia jambo hili na namshukuru sana Mheshimiwa Mavunde amenipa ushirikiano mkubwa maana Wilaya yetu ilikuwa hata Afisa Kazi hakuna lakini ameniahidi na amekuwa akimpa maelekezo Afisa Kazi yule ili kuweza kuja kutatua matatizo haya. Kwa hiyo, naomba muendelee kutusaidia maana wananchi wetu wanapata tabu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili katika eneo hili, katika Jimbo langu kuna viwanda lakini wawekezaji wale wameleta wafanyakazi wenye asili ya kigeni. Watu wale wanafanya kazi ambazo zingeweza kufanywa na mwananchi wa kawaida lakini wanaachwa wanaishi kwenye ma-godown mle, hakuna Afisa Uhamiaji anayekwenda kukagua vibali vyao, hakuna Afisa Kazi, wananyanyasa Watanzania kumekuwa na matatizo ambayo yangeweza kuepukika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana eneo letu la viwanda Mbagala mfanye ukaguzi wa uhakika na wa umakini. Zile kazi ambazo zinaweza kufanywa na Watanzania wa kawaida wazifanye na hao wageni watafutiwe maeneo mengine ya kuweza kufanya kazi. Japokuwa tunataka teknolojia na maendeleo lakini nchi yetu isiwe jalala la kufanya watu waje tu kufanya kazi ambazo hata Watanzania wa kawaida wanaweza kuzifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo nije vilevile kwenye ajira za Walimu. Katika suala hili la ajira za Walimu kuna malalamiko mengi. Malalamiko haya yanatokana na kutopandishwa vyeo kwa muda mrefu na wanapandishwa vyeo lakini hawalipwi stahiki zao. Leo asubuhi limeulizwa swali na Mheshimiwa Naibu Waziri amelijibu, imefika mahali Walimu wamefanya kazi ya kusahihisha mitihani hawajapewa malipo yao. Yametoka maelekezo mikoa ilete, imeleta mikoa tisa kwa mujibu wa Mheshimiwa Waziri lakini hao waliochelewesha kuleta hawakutumbuliwa majipu na wameongezewa muda mpaka Jumatatu kama nimemsikiliza vizuri Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, madai ya Walimu yako mengi, matatizo ya Walimu yako mengi na kero za Walimu ziko nyingi. Mheshimiwa Waziri Mkuu wewe ulikuwa Mwalimu unajua changamoto zinazowakabili Walimu nchi hii, jitahidi kuhakikisha Walimu wanapata stahiki zao kwa wakati, wale wanaostahili kupandishwa vyeo wapandishwe vyeo kwa wakati na vile vile malipo yao yafanyike kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile niipongeze Serikali hii, leo tuna Waziri anayeshughulikia ulemavu. Napenda kuipongeza Serikali kwa sababu hapo nyuma ilikuwa inaonekana walemavu ni kama watu walioshindwa maisha, wasiokuwa na mwelekeo, walikuwa wanatengwa lakini baada ya kuteuliwa tu Mheshimiwa Possi amefanya ziara kuangalia vyuo vya walemavu, amezunguka kuangalia changamoto na matatizo ya walemavu, nampongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana waendelee kuimarisha kambi zile za walemavu mfano kule Nunge Kigamboni na Mbagala eneo la Chamazi kuna kambi ya Muhimbili. Kambi ile ilikuwa inawaweka wale walemavu wa matatizo ya akili na mambo mengine, lakini sasa hivi haina huduma zozote, eneo lake limeanza kuvamiwa na matokeo yake inakuwa ni maficho ya wahalifu. Ningeomba sana Mheshimiwa Possi na hili alitazame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia ni kwenye elimu, Jimbo langu ni jipya ambalo lina wakazi zaidi ya watu laki nane. Baada ya kuanzishwa elimu bure kuna mfumuko mkubwa wa wanafunzi. Nitatolea mfano Shule ya Msingi Mbande iliyoko Kata ya Chamazi tuna wanafunzi wa darasa la kwanza 1,375; Shule ya Msingi Majimatitu nina wanafunzi elfu moja na mia mbili kadhaa. Juhudi zimekuwa zikifanywa na Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya lakini tunaomba Ofisi ya Waziri Mkuu itutazame kwa jicho la huruma sana. Jimbo la Mbagala limeelemewa na idadi kubwa ya wanafunzi na halmashauri ile uwezo wake ni mdogo. Kwa hiyo, naomba sana ndugu zangu Ofisi ya Waziri Mkuu mtuangalie kwa jicho la huruma kwa kutuongezea ruzuku, ushauri na ufundi na kwa jinsi mtakavyoweza kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoke hapo niende kwenye suala la maji. Nimesikia programu nyingi sana za maji lakini hakuna hata moja iliyogusa Jimbo la Mbagala na Wilaya ya Temeke. Ukisikia programu Ruvu Juu inakwenda Kimara, Changanyikeni na maeneo mengine. Kulikuwa na mradi wa Kipera, Mkuranga na mradi wa Kimbiji, huu sasa ni mwaka wa nane haujatekelezwa na hatujapata maji hayo yanayotoka katika vyanzo hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisema hapa kuna Mto Rufiji unao uwezo wa kuchangia upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo mengi ambayo mradi huu wa maji unaweza ukapita kama ukiwekewa msisitizo. Mfano ukitoa maji Mto Rufiji yatapita Ikwiriri, Kibiti, Bungu, Jaribu, Njopeka, Kimanzichana, Mkuranga yenyewe, Vikindu, Kongowe, Mbagala, Temeke na maeneo mengine ya Jiji la Dar es Salaam. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Maji hebu angalia jinsi gani unavyoweza ukaanza mchakato wa kutuletea maji kupitia Mto Rufiji na vile vile mradi huo wa Kipera, Kimbiji nao utekelezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba Mbagala sasa hivi ina wakazi karibu laki nane, maji ni ya kisima. Mbagala ina viwanda, maji ni ya visima, je, mnatuweka katika kundi gani? Maana walioko pembezoni ya nchi wanasema wamesahauliwa, jamani Mbagala iko Dar es Salaam, tumekosa nini kule hatuna maji safi na salama? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie kwenye suala la ulinzi na usalama. Mbagala sasa hivi imekuwa wilaya lakini Kituo cha Polisi kinachotumika kama wilaya hata Police Post haistahili lakini Askari wetu kule sasa hivi wanatafuta bodaboda kwenye mitaa na mitutu ya bunduki, usiku wamelala, uhalifu unafanyika sana usiku hakuna misako, hakuna doria.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Siku hizi Tigo wamekuwa kazi yao kukamata pikipiki mpaka mitaani zamani walianzia jijini katikati kule sasa wamekuja kwenye maeneo yetu ya mitaa. Kama kuna matatizo na maelekezo wapeni madereva wajielewe na waelewe, kama kuna elimu wapeni, wapewe leseni wafuate utaratibu, hawajakataa kufuata utaratibu lakini haya yamekuwa ni manyanyaso na kero kubwa. Naomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu hili nalo ulitazame na utoe maelekezo mahsusi juu ya madereva wa bodaboda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wastaafu nao jamani wamelalamika sana nchi hii. Kila tukija kwenye Bunge kuna kero za wastaafu, hebu tumalize na hili nalo ni jipu, walipwe stahiki zao. Juzi Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza vizuri, kuna mchakato wa kuwaongezea zile pesa zao laki moja kutoka elfu hamsini lakini hata hiyo elfu hamsini maeneo mengine hazifiki, hebu angalieni jinsi gani ya kuwasaidia wastaafu hawa. Wapo wastaafu ambao wamestaafu jeshini, Walimu na watumishi wengine katika kada mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mradi wa REA. Jimbo langu la Mbagala katika Kata ya Tuangoma, Chamazi na maeneo mengine yalipata mradi huu, nguzo sasa zimelala barabarani mwaka, miezi sita, waya hakuna, hakuna Mkandarasi, Wizara imekaa kimya na tunategemea Julai tunaanza mradi mpya, phase III, hebu hii phase II basi muisimamie maeneo yetu yapate umeme. Sambamba na hilo kuna low voltage. Mbagala ikifika saa 12 huwezi kuwasha fridge, kupiga pasi na kusikiliza redio na TV, umeme ni mdogo. Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini hebu tuangalie Mbagala kwa huruma, tuweze kupata umeme wa kutosha na wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niseme jambo moja. Hotuba hii ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu huna pa kuikosoa, imejielekeza katika kila eneo. Kwa hiyo, ninachoomba ni usimamizi ili yale ambayo tumeyakusudia yaweze kutekelezeka. Pili, wengi wanasema, Upinzani wanasema hivi, mimi sitaki kuwasema Upinzani, tulishasema toka kwenye kampeni tumejipanga na wataisoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Majaliwa ametokea tangu Mwalimu, ametokea kwenye utumishi sasa ni Waziri Mkuu utamdanganya nini kwenye utumishi wa umma? Siyo hilo tu, Naibu Waziri, Mheshimiwa Mavunde alikuwa Mwenyekiti wa Vijana anawajua vijana na anajua mazingira ambayo anatakiwa ayatumikie, leo utasema nini na utamkosoa nini? Mheshimiwa Dkt. Possi ameshakuwa Mwalimu UDOM na maeneo mengine nje ya nchi amefundisha, leo ni Waziri anayeshughulikia walemavu utamdanganya nini, utamkosoa wapi? Mama Jenista Mhagama ninyi wenyewe mnamfahamu na mnamjua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme kwamba, tukijipanga vizuri siyo watasusia tu, watakuja kutaka ushauri kwetu na tunawakaribisha na tutawasikiliza ili tuweze kulipeleka mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, juzi amefungua Daraja la Kigamboni, lakini pale pale baada ya kufungua daraja lile ameona kutakuwa na changamoto ya foleni. Kwa hiyo, amesema kabisa zijengwe njia sita kutoka Rangi Tatu mpaka Gerezani. Niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ahadi ile ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa pale isimamiwe kwa haraka ili kupunguza kero ya foleni kutoka Mbagala kuingia katikati ya mji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kuna barabara inayotoka Charambe kwenda Chamazi mpaka Msongola. Barabara ile iliwahi kuleta kashfa katika Serikali ya Awamu ya Pili na baadhi ya Mawaziri wa Awamu ya Tatu wakaenda Mahakamani, lakini mpaka leo haina marekebisho hasa kipande cha kutoka Kwa Mbiku mpaka Mbande haipitiki kabisa. Naomba sana Waziri wa Ujenzi katika majumuisho yake atujibu hili, imekuwa ni kero na ni tatizo kubwa. Ile barabara haina vituo vya basi, haifanyiwi matengenezo na imekuwa ni mahandaki matupu. Naomba sana Mheshimiwa Waziri ututazame kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nipongeze sana Chama chama Mapinduzi kwa Ilani nzuri inayotekelezeka na inayoeleweka. Huwa wanasema Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi mnaahidi hamtekelezi, wameahidi Daraja la Kigamboni juzi tumefungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine, labda uelewa wangu mdogo. Mheshimiwa Rais alifuta Sherehe za Uhuru akasema pesa hizi ziende kutengeneza barabara ile ya Mwenge. Leo watu wanasema anatumia pesa vibaya, pesa zile hazijaidhinishwa, kwani jamani Wapinzani wamekuwa CAG wa nchi hii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Bunge limetoa pesa kwa ajili ya utengenezaji wa madawati, ooh allocation ya ile pesa imeidhinishwa na nani, CAG atasema, kama kuna misallocation atasema jamani mlichofanya siyo. Leo wameanza wao kukosoa, si kwamba wanakosoa wanaona sasa hivi foleni hakuna kabisa barabara ya Mwenge kwenda katikati ya mji, kwa hiyo, hawana cha kusema na kama hawana cha kusema tutatafuta mengine ya kusema na tutawapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni demokrasia na utawala bora. Wanajua leo sisi tuna Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, tumetoka tangu Awamu ya Kwanza ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wao wana awamu ngapi hata ya uongozi wa kwenye chama? Kwa hiyo, chama chetu kina demokrasia na tunakubali kukosolewa, tunajikosoa, tunasonga mbele na tutaendelea kusonga mbele Watanzania wanatuamini na wanakiheshimu Chama cha Mapinduzi kimekuwa chama cha mfano wa kuigwa Barani Afrika na dunia kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nichukue fursa hii kuunga mkono hoja na niwapongeze sana Mawaziri kwa ushirikiano wanaotupa, hakuna matabaka, wamekuwa wasikivu na tutaendelea kuwaombea Mungu mfanye kazi zenu ili nchi yetu isonge mbele. Matatizo na changamoto zipo, naamini kwa Serikali hii ilivyojipanga tutayatatua na tutakwenda tunapopahitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu unajielekeza katika eneo la viwanda vidogovidogo kwani eneo hili likisimamiwa na kupewa kipaumbele litachochea na kukuza ajira, Wizara isimamie SIDO kuanzisha mitaa ya viwanda, mfano katika Jimbo la Mbagala Kata ya Chamazi, Charambe, Tuangoma, Kilungule na Kiburugwa zina maeneo ya kutosha kwa
ajili ya mpango huo, kutokana na idadi kubwa ya watu katika Jimbo langu naomba mpango huo utambuliwe na Wizara na kuanzishwa kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Pili; mchango wangu unajielekeza katika uwezeshaji wa wajasiriamali wa kati na wa chini kabisa. Uwezeshaji huu utasaidia sana kuinua kipato, pia uwezeshaji wa zana kwa ajili ya kuanzisha viwanda vidogovidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tatu; Wizara ifanye uhakiki wa viwanda vilivyobinafsishwa kama vinafanya kazi kwa malengo yaliyokusudiwa kwani viwanda vingi vimebaki kuwa maghala na magofu mfano TANITA kiwanda kilichopo Mbagala kimegeuzwa ghala la kuhifadhia chupa chakavu. Serikali ikirejeshe kiwanda ili kiweze kuendelezwa kwa madhumuni yaliyo kusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Nne; kumekuwa na ongezeko kubwa la viwanda vidogo vidogo vilivyoanzishwa lakini vimekuwa hatarishi katika mitaa na maeneo ya makazi. Wizara ihakiki viwanda hivi ili visilete madhara katika jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tano; Wizara iangalie uwezekano wa kuisaidia Halmashauri kujenga na kuboresha masoko yawe ya kisasa ili kutoa huduma bora na masoko yawe ya kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sita; Wizara ina hakika gani kupitia TBS kuhakikisha kuna mawakala wa ukaguzi wa bidhaa nje ya nchi mfano magari yaliyopo Uingereza, Japan, Dubai na kadhalika. Uhakiki wa mapato, ubora wa uhakiki huo, umakini na uaminifu wa mawakala hao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, natanguliza shukrani, nawasilisha.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie bajeti hii ya Serikali. Mchango wangu ningeomba niondolewe mashaka na namtaka Mheshimiwa Waziri anijibu mashaka haya kwa sababu tuna-experience na jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la property tax Halmashari zote tatu za Jiji la Dar es Salaam tuliwahi kukusanya mapato kwa mfumo huu lakini TRA walichukua chanzo hiki cha mapato, kukawa na ugumu mkubwa sana wa Serikali kurejesha au TRA kurejesha zile pesa kwa Halmashauri. Kama wakituthibitishia kwamba sasa hivi wamejipanga na wanaweza kuzirejesha pesa hizi kadri wanavyokusanya sisi tutaunga mkono hoja, hatuna hoja na hilo. Suala la kuchukua chanzo hiki na kuanza kuomba misaada mtakuwa mnatuonea, yaani itakuwa kama tunaomba na hii ipo katika maeneo mengi siyo kwenye property tax tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nina mfano wa barua ambayo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke inaomba gawio la asilimia 30 kutoka Wizara ya Ardhi ya kodi ya ardhi karibu shilingi bilioni moja tangu mwaka jana mwezi wa nne mpaka leo, hata majibu ya kusema tumepokea barua wameshindwa kutoa. Siyo kwamba tunaomba msaada ni haki yetu, Halmshauri ina majukumu mengi inashindwa kutekeleza wajibu wake hatuna barabara, hatuna maji, hatuna hospitali lakini Wizara imekuwa si sikivu. Kwa hiyo, sisi tunachomba kama TRA wanapewa jukumu hili basi hizi pesa zirudi kwa wakati ili zilete maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile kuna tatizo kubwa sana ambalo nimeliona la Serikali Kuu kutopeleka pesa za maendeleo kwenye Halmashauri zote nchini. Unakuta Accounting Officer pale, Mkurugenzi anasubiri disbursement kutoka Hazina miezi sita mpaka nane, matokeo yake inaiba vifungu vingine baadaye inaleta query kwa CAG. Kama Serikali imejipanga kutatua kero za wananchi basi pesa zipelekwe katika maeneo husika kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Mbagala ni jpya lakini kongwe kutoka Jimbo la Kigamboni. Jimbo letu tuna tatizo kubwa sana la barabara ambazo zimekuwa hazipitiki, maeneo mengine yamejifunga. Ukitoka pale Zakhem kwenga Kingugi lazima uzunguke, ni eneo la kwenda kama mita 500 unatumia kilometa tatu, barabara mbovu haipitiki na tumekuwa tukiomba lakini haijashughulikiwa. Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi imeizungumzia na Mheshimiwa Rais alivyokuja wakati wa kampeni pale Zakhem alituahidi, naomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kutimiza ahadi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile barabara ya kutoka Mtoni Kijichi kwenda Zakhem eneo la Mbagala Kuu imeharibika kabisa na hii ilikuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwamba barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Cha kusikitisha ni barabara ya kilometa mbili tu lakini mwaka huu imetengewa robo kilometa itengenezwa na TANROADS, huu ni utani. Rais alishaahidi, Serikali ilishasema itatekeleza, naomba Waziri mhusika atilie mkazo mwaka huu barabara ile iweze kuisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni la Hospitali ya Zakhem. Hospitali hii ina mkusanyiko mkubwa wa wagonjwa na inahudumia watu wengi lakini Serikali ilisema italipa fidia ili iweze kuchukua lile eneo lakini mpaka leo imekuwa ni hadithi. Naomba Serikali ije na majibu ya jinsi gani ya kuweza kupanua hospitali ile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, lilitoka tangazo la Serikali kusema kwamba Wizara sasa imepandisha hadhi hospitali zile tatu za Mkoa wa Dar es Salaam za Amana, Temeke na Mwananyamala kuwa hospitali za Mkoa.
Huu mwaka wa saba sasa hivi Halmashauri bado zinazihudumia, Serikali imekwepa jukumu lake la kuchukua zile hospitali na kuzihudumia. Sasa tunaomba Serikali Kuu ichukue zile hospitali ili Halmashauri hizi ziweze kujipanga na kupeleka huduma mpaka chini. Wananchi wanapata taabu, tunazungumzia zahanati kila kijiji sisi hatuhitaji zahanati kila kijiji tunataka tuwe na hospitali inayohudumiwa na Halmashauri ipasavyo ili wananchi wetu waweze kupata huduma stahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, katika maboresho ya afya, eneo la Mbande hospitali ile sasa hivi imeelemewa. Tunaomba Serikali iongeze ruzuku kwenye hospitali ile ili ule upanuzi tulioahidiwa uweze kufanyika wananchi waweze kupata huduma za afya safi na za uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo ambalo ningependa sana kulizungumzia kwenye Jimbo langu la Mbagala nalo ni suala la ulinzi na usalama. Serikali ilianzisha Mkoa wa Kipolisi wa Temeke lakini huu sasa ni mwaka wa saba hakuna kituo cha polisi hata kimoja ambacho Serikali imesema sasa baada ya kuanzisha Mkoa wa Kipolisi Wilaya ya Mbagala ina kituo cha polisi, ina kituo cha OCD na huduma zingine zinazostahili. Vile vituo ambavyo wananchi walivijenga ndiyo vinaitwa police post lakini vinafungwa saa tisa, mwanzo wa uhalifu vituo vinafungwa na unakuta kuna askari mmoja. Mbagala kuna tatizo kubwa sana la uhalifu wote mnafahamu, naomba Serikali ilitazame kwa jicho la huruma eneo la Mbagala.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuzungumzia maboresho ya Mahakama. Tunasema tutoe haki lakini leo Mbagala ina Mahakama ya Mwanzo moja inayohudumia wananchi karibu 800,000 haki inapatikana vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile ili uweze kupata haki Mahakama ya Wilaya mpaka uende Temeke. Temeke yenyewe ina Jimbo la Temeke, Kigamboni inategemea Temeke, hatuna Mahakama. Leo tungekuwa na Mahakama Tuangoma, Mbande na maeneo mengine ingetusaidia kuharakisha kesi kumalizika kwa haraka. Kwa hiyo, naomba Serikali Kuu nayo ilitazame suala hili na kutusaidia kupata haki katika eneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende haraka haraka kwenye huduma za nishati ya umeme. Kuna mradi wa REA ambao ulikwenda katika maeneo ya Chamazi, Kwamzala, Mbande, Kwa Masista lakini wale wakandarasi wametupa nguzo wameondoka mpaka leo wameingia mitini. Sijui Waziri anatujibu nini kuhusiana na jambo hili kwani limekuwa kero kubwa maana Mbagala tupo Dar es Salaam lakini umeme hakuna.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna suala la low voltage. Jimboni kwangu ikifika saa 12 huwezi kuangalia televisheni, huwezi kuwasha friji kwa sababu umeme ni mdogo mno. Tunasema sasa tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda tunakwendaje nao ikiwa tuna low voltage Mbagala? Mbagala tuna eneo la viwanda lakini bila tatizo hili kushughulikiwa suala la viwanda litashindikana.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna kero kubwa ambayo wananchi wa Mbande wanailalamikia ni suala la Kilwa Energy. Huu sasa mwaka wa saba au wa nane hawajalipwa fidia na wameambiwa wasifanye shughuli zozote katika eneo unapopita ule mradi, hawa wananchi wanakwenda wapi na mbona hawalipwi?
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimeongea na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati ananiambia wanategemea kupata pesa kutoka TIB. Kila siku wananchi wanaahidiwa kama hakuna pesa waambieni hakuna waendelee na shughuli zao za maendeleo. Kama pesa zipo walipeni waondoke pale kuliko kuendelea kuwanyanyasa na kuwasumbua pasipo na sababu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi kero zingine zinawezekana kumalizika. Maana ile Kilwa Energy inaanzia Somanga inakuja mpaka Mkuranga pale kwa Mheshimiwa Ulega, inakuja mpaka Mbagala, imekwenda mpaka Ilala ni tatizo. Mpaka watu washike mabango na waandamane ndiyo muelewe kama watu wanakerwa? Naomba Serikali kidogo ijirekebishe na iweze kutekeleza kwa wakati lile inaloahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la nishati kumekuwa na tatizo na Mheshimiwa Waziri katusomea bajeti yake kwamba gesi imepanda. Hata hivyo, gesi hii tunayoitegemea inatoka nje ile gesi ya Mtwara na maeneo mengine tunayoambiwa kila siku inakuja inakamilika lini ili Mtanzania wa kawaida aweze kutumia gesi maana maeneo yetu yale ukikamatwa na mkaa ni kesi. Sasa basi kama ni hivyo tupate nishati mbadala ya gesi, gesi yenyewe haipatikani na mnazidi kuipandisha bei. Naomba kama gesi ya Mtwara na Lindi bado haijapatikana, tupunguze tozo katika gesi wananchi waweze kupikia gesi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa vilevile kuzungumzia suala dogo tu maana najua kengele inaweza kugonga, kuna suala la mradi wa njia sita kutoka Bendera Tatu au pale BP mpaka Mbagala. Hii barabara ni muhimu sana kwa sababu wakazi wa Mbagala tunategemea na tunatarajia DART Phase II ije lakini ije kwa haraka na njia zile ziweze kupitika. Kumekuwa na msongamano na kumekuwa na matatizo makubwa, jioni kuna foleni, asubuhi kuna foleni. Kwa hiyo, kama mchakato huu upo uanze haraka ili wananchi na wao waweze kwenda na mwendo kasi kama ilivyo katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naona kuna tatizo kidogo la ufundi, katika mradi huu feasibility study ilifanyika miaka 10 iliyopita ndiyo maana ule mradi uliishia Kimara pale lakini mahitaji kwa Kimara pale siyo peke yake, Mbezi Kiluvya, Kibamba wote walikuwa wanahitaji. Kwa kule Mbagala mradi huu ulikuwa unaishia Rangitatu, DART wanataka kulipa fidia mpaka viwanda, kwa nini tuondoe viwanda ikiwa tuna uwezo wa kuusogeza mradi huu? Ileile fedha ya fidia ingetumika wangekwenda mpaka Kongowe eneo la Mwandege pale kwa Mheshimiwa Ulega, lile pori sisi kwetu ni kero, wahalifu wanajificha pale. Ondoeni lile pori wekeni kituo cha mabasi ya kisasa, wanaotoka mikoani wataishia pale, wanapanda mabasi ya mwendokasi wanakwenda katikakti ya mji na maeneo mengine. Ni suala la kukubaliana tu, si lazima kwamba feasibility study iliishia Rangitatu basi lazima tuishie Rangitatu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile barabara ya kutoka Charambe kwenda Mbande iliwahi kuleta kashfa tangu Serikali ya Awamu ya Tatu na kuna baadhi ya Mawaziri walipelekwa Mahakamani. Barabara ile haina vituo, haina mifereji ya kuweza kuwafanya watu wakapita vizuri na haipitiki wakati wa masika…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kupata nafasi ya kuchangia taarifa hizi za Kamati mbili. Lakini, maji na chai peke yake havitoshi Wajumbe wa Kamati hii tunataka oversight ili tukaikague Serikali vizuri hasa Serikali za Mitaa. Lakini maji peke yake na hivi vitabu mama yangu Rwamlaza amesema pale vinatuzidi umri…
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo nitalifafanua mbele, lakini ningependa nianze kwa kushukuru kunipa fursa hii na mimi kuweza kuchangia. Na mimi moja kwa moja wenzangu wengi wamezungumza mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Wenzangu wengi wamezungumza kwa masikitiko makubwa jinsi gani Serikali yetu inavyoweza kuchangia kuzorotesha maendeleo katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hayo kwa sababu wengi wamezungumza, Serikali imekuwa ikichelewa sana kupeleka fedha za maendeleo katika Halmashauri hizi, lakini tunapouliza maofisa kutoka Hazina wanakuwa hawana maelezo na sababu za msingi. Kwa hiyo, ningeomba Waziri wa Fedha atujibu na atueleze tatizo ni la kibajeti au kuna uzembe na hao wazembe wanachukuliwa hatua gani kwa sababu watendaji wetu huko chini wanaumia sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Halmashauri hasa za pembezoni, mfano Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo kwa kipindi kirefu haikupelekewa fedha kabisa za maendeleo. Lakini kama walivyosema watangulizi wangu waliozungumza hapa, maagizo yanatoka, tujenge maabara, tufanye shughuli mbalimbali, mwenge na mambo mengine; kwa hiyo, Afisa Masuuli inabidi achambuechambue vifungu kuweza kukamilisha yale ambayo yameagizwa. Kama hizi fedha haziwezi kwenda kwa wakati ni kweli kabisa na usahihi tunaziua hizi Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini lengo la Serikali ni jema, inawezekana katikati hapa kuna vitu ambavyo vinasababisha hizi fedha zisiende. Kwa hiyo, Serikali iwe makini kupeleka hizi fedha za maendeleo kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile suala la hizi Kamati, tumeomba muda mrefu kwenda oversight ili tuweze kukagua, kwa sababu tunachoandikiwa kwenye vitabu sicho kile ambacho kiko katika site. Kwa hiyo, tumeambiwa kibali hakijatoka fungu halijaingia. Lakini kama mtakumbuka Waheshimiwa Wabunge wenzangu, Mheshimiwa Rais alisema tumsaidie kazi ili aweze kupambana na ufisadi katika nchi hii. Leo tunawekwa katika chumba kimoja tupewe maji au chai tunamsaidiaje kazi tukiwa ndani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba Serikali ione haja ya kuziongezea bajeti hizi kamati ili twende kufanya oversight kukagua miradi ya maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nirudi moja kwa moja kwa Mkoa wangu wa Dar es Salaam, haswa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam. Kwa sisi watu wa Dar es Salaam Halmashauri ya Jiji kwetu ni tatizo. Na ningeomba Waziri uangalie muundo wa Jiji kama ikiwezekana basi tuvunje lile jiji kwa sababu sasa hivi tuna Halmashauri tano za Manispaa za Jiji la Dar es Salaam. Kwa sababu katika kitabu hiki cha LAAC ukurasa wa 28…
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilichokuwa naeleza East Africa Meat Company Limited, imezungumzwa hapa tatizo lake. Tumegawanya rasilimali katika hizi Halmashauri, lakini hili deni au hizi fedha ambazo Halmashauri zote hizi zilichangia kwenda Jiji hatujagawana wala hatujaambiwa na Serikali kwamba hizi fedha ziko wapi? Halmashauri ya Temeke, Ilala, Kinondoni zilitoa fedha kuchangia katika mradi huu, na ni pesa nyingi sana billions of money.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mpaka leo Jiji halijaelezwa kwamba hizi fedha ziko wapi, Halmashauri hizi zitafaidika na nini. Leo kwa Jiji kazi iliyobaki kwake ni sera, lakini sera iliyokuwepo pale kwa wengi wa Dar es Salaam tunaona ni kuongeza parking wasizozianda. Jiji pale kazi yao kubwa ni kukamata bodaboda kuwapa majembe na kampuni zingine hakuna kazi zinazofanywa na Jiji, zinaingilia mpaka maeneo ya Halmashauri zetu, ndio maana tunasema Jiji sasa hivi halina kazi. Lazima tuseme ukweli, tusifichane, jiji bora livunjwe ili Halmashauri ili zipate uwezo na Serikali ipunguze mzigo mkubwa wa kulilea Jiji ili Halmashauri mpya na zilizokuwepo za zamani. Huo ndio ushauri wangu kwa Serikali na ninaamini mtazingatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie hii East African Meat kuna ardhi pale ambayo ipo. Ardhi ile sasa hivi imegeuka kichaka, haijaendelezwa bora Halmashauri ya Ilala ipewe lile eneo waweze kuendeleza au kujenga shule na shughuli zingine za maendeleo kuliko vile lilivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile nizungumzie suala la watumishi katika maeneo ya pembezoni. Hivi leo kuna haja gani eneo kama la Kariakoo kuwa na Afisa Kilimo au Afisa Mifugo, au Upanga? Mfano kwenye Halmashauri yangu ya Temeke pale Afisa Kilimo hakuwa na bajeti amekaa mwaka mzima analipwa mshahara wa Serikali. Lakini Kalambo kule tuliona Afisa Mipango Miji ndio ana kaimu kuwa Afisa Kilimo, watu wako Dar es Salaam kule hawafanyi kazi, wanalipwa mishahara, maeneo ya pembezoni watu wa kufanya kazi hizi hawapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasikia Wabunge wenzetu wa pembezoni wanalalamika kuwa Maafisa Ugani hawapo, lakini Dar es Salaam wapo. Sio hilo tu, Wabunge wengi hapa wamezungumzia na wamelalamika suala la kukaimu watu ukuu wa idara. Lakini katika Halmashauri zetu za Dar es Salaam unaweza ukakuta idara moja ina maofisa zaidi ya sita, hawana shughuli ya kufanya zaidi ya kusubiri semina. Kwa nini wanakaa Dar es Salaam kule, waende maeneo mengine wakalitumikie hili Taifa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mgawanyo wa rasilimaliwatu lazima uzingatiwe. Wataalam waende kwenye maeneo yenye mahitaji ili waweze kutusaidia kusukuma gurudumu la maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba sana suala la mradi wa mabasi yaendayo kasi ambayo unasimamiwa na DART, mara nyingi nikipita pale TAZARA huwa nashangaa kidogo, ule mchoro unavyoonesha kwa sababu DART Phase II, utagusa eneo la Gongo la Mboto kupita TAZARA mpaka Kariakoo. Lakini ule mchoro wa interchange pale hauoneshi kama zimetengwa tayari, eneo la barabara za mwendo kasi. Kwa hiyo tunategemea mwakakni tukianza kutekeleza huu mradi, tuvunje tena. Kwa hiyo, naomba Serikali itupe majibu je, pale wana mpango gani au huu mradi tena umeshakufa umeishia pale ulipo?.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa eneo la Mbagala, Mheshimiwa Mwijage anasema kila siku hapa tunataka kuimarisha viwanda, tunataka kufufua viwanda. Eneo ambalo DART wameamua ku-plan kwa ajili ya kulipa fidia zaidi ya bilioni 186 ni eneo la viwanda ambavyo vingine vinazalisha. Lakini ukitoka kilometa sita kutoka pale Mbagala Rangi Tatu kwenda mpaka Kongowe kuna msitu mkubwa umejaa pale hauna kazi yeyote, kwa nini wasi-extend mpaka kufikisha pale vikindu ule msitu, hauna kazi yoyote zaidi ya kuwa maficho ya majambazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru Mheshimiwa Waziri Maghembe ametoa heka pale ambazo zile zingesaidia ile DART wangei-extend ili Serikali isipoteze fedha nyingi ya fidia ikiwa eneo lipo. Ningeomba sana Mheshimiwa Simbachawene watu wa DART walitizame hili kuliko kupoteza fedha pasipokuwa na sababu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wengi wamezungumza kuhusu CAG, ni kweli CAG anafanya kazi katika mazingiara magumu sana. Naomba Serikali hii ya Awamu ya Tano yenye nia njema ya kumkomboa Mtanzania wamuwezeshe CAG aweze kufanya kazi. Bila kufanya kazi CAG Kamati hizi zinakuwa hazina macho kabisa na zinakuwa hazina uwezo wa kutekeleza majukumu yake. Lakini nimuombe Waziri wa Fedha, nina taarifa Halmashauri zetu Dar es Salaam bado hazijapata gawio la property tax. Na hata hao TRA wenyewe wanasema ndiyo kwanza wanaanza kujipanga na kutoa semina ili waanze kukusanya mapato. Ndugu zetu mmetuchukulia chanzo hiki kikubwa kwa Halmashauri za Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Serikali inashindwa kuleta hizi fedha mnategemea tutekeleze vipi miradi ya maendeleo, mnategemea tujiendeshe vipi? Kama jukumu hili mmelishindwa naomba mrudi nyuma, mjisahihishe mtuachie Halmashauri tukusanye property tax ili tuweze kutekeleza miradi yeti ya maendeleo. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, Sheria ya Manunuzi ya Umma (Public Procurement Act) ni tatizo katika Halmashauri zetu, zinachukua muda mrefu procedure hizi mpaka kuweza kutangaza mzabuni. Lakini huyo mzabuni anayepatikana, anapatikana kwa gharama kubwa, naomba sana Serikali ifanye marekebisho ya sheria ili sheria hii iweze kutusaidia, isiwe kikwazo katika kutekeleza miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna kero kubwa ya uhakiki wa madeni ya walimu, hasa waliosahihisha mitihani ya darasa la saba na darasa la nne. Walimu hawa hawajalipwa muda mrefu, wamekuwa wakilalamika na kila wakija Wakurugenzi wanasema fedha hazijatoka kutoka Hazina hazijaletwa kutoka Serikali Kuu. Naomba Serikali iangalie kwa jicho la huruma walimu hawa ambao wanatusaidia kuboresha elimu ya watoto wetu na wao ni watumishi wanastahili kupewa haki, kwa wakati ili waweze kuwa na moyo na morali wa kuweza kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine ningependa kulizungumzia na nitatolea mfano Halmashauri ya Jiji au Mji wa Iringa. Walikuwa na mpango na mwekezaji wa kuwekeza katika eneo la machinjio na kituo cha mabasi, lakini wamepeleka Wizarani karibu miaka minne sasa hivi hawajapata majibu na sisi Temeke pia tumepeleka Wizarani project zetu, lakini mpaka leo hatujapa kibali cha Waziri husika na ushauri wa CAG. Kwa hiyo, ile miradi baadaye inakuja ina-collapse Halmashauri zinashindwa kuwekeza.
Kwa hiyo mimi ningeomba sana Serikali ibadilishe utaratibu, ili Halmashauri hizi zikiwa na plan ya kuwekeza basi uwekezaji ule ufanyike kwa haraka na wapate ridhaa ya Waziri na wahusika kwa haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile suala la Mifuko ya Hifadhi za Jamii. Jamani wastaafu wetu wanateseka sana, hawapewi mafao yao kwa wakati, tangazo la nyongeza ya Serikali mpaka sasa hivi hakuna na majibu yanakuwa hakuna na hawa watu ni wastaafu, wanachotegemea ndicho hicho hicho kilichokuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hapa nimesoma ripoti ya PAC Serikali inadaiwa pesa nyingi sana na Mifuko ya Hifhadhi za Jamii. Lazima tuseme ukweli kama hili ni tatizo basi Serikali ijipange, Mifuko ya Hifadhi za Jamii iwe inalipwa at least nusu ya madeni yao ili waweze kujiendesha na waweze kulipa madeni yao mbalimbali ikiwemo pamoja na kuwalipa wastaafu.
Mheshimiwa Naibu Spika, wastaafu wanahangaika sana, wastaafu wanapata shida sana. Mimi ningeshauri sana Serikali iwaangalie wastaafu kwa jicho la huruma.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile limezungumzwa hapa kwa upana sana suala la UDA. Ni kweli UDA ina kigugumizi na hatujapata majibu yake, lakini sisi tuombe Halmashauri zetu nazo zinatakiwa zipate zile unallotted share basi na sisi tuelekezwe jinsi gani ya kuzipata ili tuweze kumiliki. Lakini sio hilo tu kuna suala la pesa ambazo ziko mpaka sasa hivi benki, kama ni ndogo kaeni fanyeni negotiation na mwekezaji, ziongezeke au kama mwekezaji hatakiwi tupewe taarifa hizi ili zile pesa kama inawezekana basi zitumike kwenye miradi ya manendeleo katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hilo tu kuna suala la pesa ambazo ziko mpaka sasahivi benki. Kama ni ndogo kaeni fanyeni negotiation na mwekezaji ziongezeke au kama mwekezaji hatakiwi, tupewe taarifa ili zile pesa kama inawezekana basi zitumike kwenye miradi ya maendeleo katika Halmashauri zetu na Manispaa zetu, lakini kero hii naomba iishe na hili neno liwe lilefutika kwa sababu, linawezekana na kama kukiwa na nia njema na ukweli na uwazi katika jambo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ningeomba sana, wengi wamezungumza na ni kweli sasahivi kuna mkanganyiko maana sasahivi Mbunge ukishirikiana na wananchi unaambiwa mchochezi. Mkuu wa Wilaya anataka wewe uende pale umpigie salute. Ni vizuri mkawapa semina Wakuu wetu wa Wilaya, mkawapa semina viongozi wetu ili wajue mipaka ya majukumu yao, wajue heshima ya Mbunge ni ipi, heshima yake yeye ni ipi na vilevile mgawanyo wa madaraka yake na majukumu yake ni upi.
Mheshimiwa Naibu Spika, isifike mahali Mbunge unaalikwa uende kwenye mahafali na Mkuu wa Wilaya mnapishana na yeye anataka kwenda kwenye mahafali. Kila mtu ana majukumu yake na katika maeneo yake. Naomba sana semina elekezi kwa viongozi wetu zitolewe ili kusiwe na mgongano. (Makofi)
Lakini lingine kumekuwa sasa hivi, hasa kwa Madiwani, nilipata taarifa kwamba kuna baadhi ya Madiwani wamekamatwa, wamewekwa ndani kisa wanaambiwa ni wachochezi. Haya mambo yanaweza yakazungumzika katika maeneo yale na yakaweza kusawazishika. Si kila jambo lazima itumike nguvu, kuna mambo ambayo tunaweza tukawaelewesha, watu wakaelewa na wakatekeleza wajibu wao na nchi yetu ikabaki kuwa salama na tukawa wamoja kwa amani na utulivu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niseme pale ambapo kuna maelewano, pale ambapo kuna maridhiano maendeleo yatapatikana. Pale ambapo kuna migongano maendeleo hayawezi kupatikana, tutumie busara katika…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono.