Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Frank George Mwakajoka (10 total)

MHE. DAVID E. SILINDE (K.n.y MHE. FRANK G. MWAKAJOKA) aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina Mpango gani wa kugenga Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Wilaya hapa Tunduma ili kuendana na ongezeko la watu na wageni wanaoingia nchini?
(b) Je, Serikali haioni vema ujenzi wa kituo hicho uende sambamba na ujenzi wa nyumba zenye gharama nafuu kwa Polisi wetu ambao wana shida kubwa ya makazi?
SPIKA: Sasa Mheshimiwa Silinde wewe Tunduma si ulishaondoka, majibu ya swali hilo Mheshimiwa Naibu, Waziri Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Hamad Yussuf Masauni. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI YA WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Kituo cha Polisi Tunduma ni kidogo na hakina nyumba za kutosha. Wilaya ya Momba inahitaji nyumba 150 ili kukidhi mahitaji ya makazi ya Askari. Kama ilivyo kwa maeneo mengi hapa nchini, changamoto kubwa ya ujenzi wa vituo vya Polisi na nyumba za askari ni uhaba wa fedha. Aidha, kwa Kituo cha Polisi Tunduma changamoto nyingine ni eneo la kufanya upanuzi wa kituo kilichopo sasa kwani kituo hicho kipo mpakani kando mwa barabara ya Sumbawanga.
Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha Jeshi la Polisi linaboreshewa makazi na kuwa na ofisi ili kuwezesha utoaji huduma kwa wananchi kuwa mzuri. Jeshi la Polisi chini ya utaratibu wa mikopo nafuu kutoka taasisi za kifedha za ndani na nje ya nchi lina mpango wa kujenga nyumba na ofisi za Polisi maeneo mbalimbali nchini. Kwa hivi sasa Serikali inakamilisha taratibu za kupata mkopo toka Bank ya Exim ya China ili kujenga nyumba 4,136 za makazi ya Askari katika Mikoa 17 hapa nchini.
MHE. PASCAL Y. HAONGA (K.n.y. MHE. FRANK G. MWAKAJOKA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya Zimamoto katika Mpaka wa Tunduma ili kuokoa mali za wafanyabiashara wanaosubiri kuvuka pindi ajali ya moto inapotokea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika Halmashauri ya Mji wa Tunduma lina kituo katika eneo la Mtaa wa Kilimanjaro, Wilaya ya Momba katika Mkoa wa Songwe kinachohudumia Wilaya zote ukiwemo mpaka wa Tunduma. Kwa sasa kituo hiki kina gari moja lililopo matengenezoni Mjini Mbeya. Hata hivyo, Askari wanaendelea kutoa Elimu ya Kinga na Tahadhari ya Majanga ya Moto na Utumiaji wa Vifaa kwa Huduma za Kwanza, sambamba na ukaguzi wa majengo na kutoa ushauri kwa wakandarasi na makampuni ya ujenzi kuhusu ujenzi bora wa miundombinu yenye usalama kwa umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kupeleka huduma ya zimamoto katika maeneo yote nchini ikiwemo Tunduma. Hata hivyo azma hii nzuri inategemea sana upatikanaji wa rasilimali fedha. Serikali itaendelea kusogeza huduma za zimamoto na uokoaji katika maeneo mbalimbali nchini karibu na wananchi kadri hali ya upatikanaji fedha itakavyoruhusu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatumia wataalam wake katika kupanga Miji na kuondokana na ujenzi holela unaoendelea nchi nzima?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu imeshaanza kushughulikia jambo hili kwa kuhakikisha kuwa katika kila Kanda tulizoanzisha tunapeleka wataalam wa kutosha wa fani zote. Hii yote ni kuhakikisha kuwa usimamizi wa uendelezaji miji nchini unakuwa katika viwango vinavyokubalika. Aidha, pamoja na jitihada hizo bado tuna changamoto kubwa ya uhaba wa maeneo yaliyopangwa na kupimwa nchini ambayo pia ni chimbuko la ujenzi holela katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto hii, Wizara yangu imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na:-
(i) Kuandaa program ya miaka mitatu ya kuandaa mipango kabambe ya Miji, Manispaa na Halmashauri za Miji yote Tanzania. Utayarishaji wa mipango kambambe ya Miji ya Mwanza, Musoma, Singida, Kibaha, Tabora, Iringa na Mtwara upo katika hatua za kutangazwa katika gazeti la Serikali ndani ya siku 90 ili watu waweze kutoa maoni yao.
Katika Jiji la Dar es Salaam zoezi hili bado halijakamilika lakini pia katika Jiji la Arusha zoezi hili halijakamilika kwa sababu zile Halmashauri hazikuelewana kwa hiyo, inabidi wakae waridhie. Aidha, katika mwaka wa fedha 2015, Wizara yangu pia ilitoa wataalam wa Mipango Miji kusaidia utayarishaji wa mipango kabambe katika Miji ya Iringa, Mtwara na Shinyanga. (Makofi)
(ii) Vilevile, Wizara imeendelea kuhakikisha kuwa kila kipande cha ardhi kinapimwa nchi nzima na Serikali imeshaanza kufanya upimaji katika Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi kupitia mpango wa Land Tenure Support Progamme.
(iii) Kuruhusu makampuni binafsi ya Mipango Miji kushiriki katika kutayarisha mipango kabambe na mipango ya kina katika miji yote nchini.
(iv) Wizara pia ilitoa wataalam katika zoezi la urasimishaji makazi katika Manispaa ya Kinondoni katika Kata za Kimara na Saranga na katika Halmashauri ya Wilaya ya Makete katika Kata ya Tandala. Katika mwaka huu wa fedha Wizara yangu inatarajia kupeleka wataalam katika Halmashauri za Manispaa ya Sumbawanga, Lindi, Kigoma Ujiji, Singida, Musoma na Tabora kwa ajili ya kuwezesha zoezi kama hilo.
(v) Vilevile kuzijengea uwezo Halmashauri nyingine ili ziweze kurasimisha maeneo yao kwa kutumia wataalam wake. Hii ni utekelezaji wa program ya miaka mitano ya urasimishaji wa maeneo ambayo hayajapangwa, ambapo Wizara yangu imeandaa mwongozo wa namna ya kufanya urasimishaji, mwongozo utakapokamilika utasambazwa katika Halmashauri zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai kwa Halmashauri zote kuandaa mipango kabambe ya maeneo ambayo yamefikia hadhi ya kuanzishwa kuwa miji ili upimaji ufanyike mapema kwa lengo la kuepusha ujenzi holela. Aidha, kwa maeneo ambayo yamejengwa kiholela Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri na wananchi wa maeneo husika tutaendelea kuboresha kwa kuyarasimisha kwa kadri ya mahitaji. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Mji wa Tunduma una vijana wengi wanaohitimu kidato cha nne lakini wanakosa nafasi za kuendelea na masomo ya juu:-
Je, Serikali inasema nini kuhusu kujenga Chuo cha Ufundi VETA ili vijana wengi waweze kupata ujuzi na kujiajiri na kuongeza kipato chao?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haitaweza kujenga Chuo cha VETA katika Halmashauri ya Tunduma kwa sasa kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Wakati juhudi mbalimbali zinaendelea za kutafuta vyanzo vya ufadhili wa kujenga Vyuo vya Ufundi Stadi kupitia VETA, wananchi wa Mji wa Tunduma waendelee kutumia vyuo vilivyopo katika mikoa jirani hususan Mkoa wa Mbeya wenye Chuo cha VETA cha Mkoa na Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) vya Nzovwe kilichopo katika Manispaa ya Mbeya na Katumba katika Wilaya ya Rungwe. Aidha, wananchi wanashauriwa kuendelea kutumia vyuo vingine vilivyosajiliwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika mikoa mbalimbali nchini ili kupata mafunzo ya ufundi stadi.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na ada ya Zimamoto ambayo wanatozwa wafanyabiashara katika Halmashauri ya Mji wa Tunduru huku kukiwa hakuna Jeshi la Zimamoto na Uokoaji eneo hilo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ada zinazotozwa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ni kwa mujibu wa Sheria Na. 14 ya 2007 ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Kanuni za Ukaguzi za mwaka 2008 na Marekebisho yake ya mwaka 2012 na 2014. Sheria na Kanuni hizi zinamtaka mmiliki wa chombo cha usafiri pamoja na usafirishaji, mmiliki wa jengo refu au fupi, chombo cha usafiri na usafirishaji, mfanyabiashara au ofisi kulipia tozo ya ukaguzi. Tozo hizo zimepangwa kutokana na ukubwa wa jengo na hatari ya moto kwenye eneo husika.
Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Momba Mkoani Songwe, Halmashauri ya Tunduma ina kituo cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ambacho kipo katika Mtaa wa Kilimanjaro na kina askari kumi na gari moja la kuzimia moto. Kwa sasa gari hilo lipo Jijini Mbeya kwa ajili ya matengenezo. Wizara kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji inafanya jitihada za haraka ili gari hilo litengamae na kurejea kituoni.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, askari wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji wanaendelea na majukumu yao mengine ya kutoa elimu ya kinga na tahadhari za moto na ukaguzi wa majengo ili kuzuia ajali za moto na majanga mengine. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 yaani Local Government Finance Act, Cap. 290, kifungu cha 6(1)(u), Halmashauri ulipo mgodi hutoza asilimia 0.3 ya mapato yote kabla ya kuondoa gharama za uzalishaji wa madini kama ushuru wa huduma yaani service levy. Aidha, kabla ya kuanza kutoza ushuru huo, Halmashauri husika inatakiwa kutunga Sheria Ndogo ya Halmashauri yaani District Council By-Laws ambazo zinaidhinishwa na Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa yaani TAMISEMI kwa mujibu wa kifungu cha 153(1) cha Mamlaka ya Serikali Mitaa yaani Local Government District Authority Act, Cap. 287.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, eneo la Halmashauri ya Tunduma hakuna leseni ya uchimbaji iliyotolewa. Hivyo, tunaendelea kuhimiza wawekezaji wa ndani na nje ili wawekeze katika utafiti na hatimaye kuanza kuchimba madini katika maeneo mbalimbali yenye madini nchini na Tunduma ikiwa mojawapo. Ahsante.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Mpemba hadi Ileje kwa kiwango cha lami ili kuunganisha na kuboresha mpaka wa Malawi na Tanzania katika eneo la Isongole?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mpemba – Isongole ambayo ni barabara kuu yenye urefu wa kilometa 50.3 inaunganisha nchi yetu na nchi jirani ya Malawi inahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Songwe. Barabara hiyo inaanzia katika Barabara Kuu ya TANZAM, eneo la Mpemba, katika Mamlaka ya Mji wa Tunduma, Wilaya ya Momba. Barabara hii ni kiungo cha kufika katika Mji wa Itumba ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Ileje na maeneo ya jirani ya nchi ya Malawi.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii kiuchumi na kijamii na kwa kuwa, ndiyo barabara inayounganisha wananchi wa sehemu mbalimbali wa Wilaya ya Ileje na nchi jirani ya Malawi na Zambia, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) inaendelea kujenga Barabara ya Mpemba – Isongole kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa utekelezaji wa mradi upo kwenye hatua za awali, zikiwemo ujenzi wa Kambi ya Mhandisi mshauri ambayo imefikia 80%, kusafisha eneo la ujenzi wa barabara kilometa 10, ujenzi wa makalvati manne na uwekaji wa tabaka la chini la barabara.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2017/2018 Serikali imetenga shilingi bilioni 4.455 kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami na katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara hii, ili mradi huu uweze kukamilika kama ulivyopangwa.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunga mkono tamko la Kilimo ndiyo Uti wa Mgongo wa Taifa kwa vitendo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Jimbo la Tunduma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu Serikali inatambua na inaunga mkono tamko la Kilimo ni Uti wa Mgongo kwa Taifa. Umuhimu wa sekta ya kilimo unajidhihirisha katika viashiria mbalimbali vya kiuchumi na kijamii kama vile mchango wa kilimo katika ajira, pato la Taifa, usalama wa chakula na malighafi za viwandani. Takribani asilimia 65.5 ya wananchi wameajiriwa katika sekta ya kilimo, asilimia 28.7 ya pato la Taifa hutokana na sekta ya kilimo, mazao ya chakula huchangia kiasi cha asilimia 65 ya pato la Taifa litokanalo na kilimo. Zao la mahindi huchangia zaidi ya asilimia 20 ya pato la Taifa litokanalo na kilimo, mazao ya chakula na biashara yanachangia asilimia 70 ya kipato katika maeneo ya vijijini. Aidha, sekta ya kilimo ni muhimu katika mikakati ya kuendeleza sekta ya viwanda nchini kwa kuchangia takribani asilimia 65 ya malighafi za viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo mikakati na mipango inayolenga kuimarisha sektya kilimo ili kuongeza tija na uzalishaji wa mazao ya kilimo pamoja na kuwapatia wakulima masoko ya uhakika. Sera, mikakati na mipango inayotekelezwa ni pamoja na Sera ya Taifa ya Kilimo ya mwaka 2013, Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya II (ASDP II) pamoja na sera, mikakati na mipango mingineyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jitihada madhubuti ya kutambua Kilimo ndiyo Uti wa Mgongo ni kuanzishwa kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ambayo inatoa mikopo ya riba nafuu ya asilimia 8 tu. Aidha, Serikali imeendelea kupunguza ada, tozo na kodi katika kilimo, kuimarisha huduma za utafiti ikiwa ni pamoja na kuanzisha Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) na kuimarisha ushirika ili uweze kuwezesha na kusimamia masoko ya mazao ya kimkakati.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatafuta masoko ya uhakika ya ndani na nje kwa wakulima wanaozalisha mazao ya chakula kama mahindi na mpunga?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia mmalaka ya maendeleo ya biashara Tanzania yaani TanTrade imekuwa ikiratibu jitihada mbalimbali za upatikanaji wa masoko ya mazao mbalimbali yanayozalishwa Nchini yakiwemo mahindi na mpunga.

Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu la utafutaji masoko ndani na nje ya nchi ikiwemo masoko ya mazao ya chakula ni jukumu endelevu. Utekelezaji wa jukumu hilo huhusisha Taasisi ya TanTrade, Balozi za Tanzania nje ya nchi, Bodi za Mazao, Soko la Bidhaa za Mazao na sekta binafsi. Lengo la kutumia Balozi zetu nje ya nchi ni kupata taarifa za kina kuhusu mahitaji ya masoko ya mazao na bidhaa za Tanzania katika nchi husika. Kwa jitihada hizo, yamepatikana masoko ya mchele na mahindi katika nchi ya Oman, Misri, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Zambia, Burundi na Visiwa vya Comoro. Aidha, kupitia TanTrade tulipokea maombi ya sekta binafsi kutoka nchi ya Rwanda ya kununua tani 102,000; nchi ya Burundi tani 100,000; Zambia tani 3000 na Visiwa vya Comoro tani 3000 za mahindi kwa kupindi cha mwaka 2018/2019. Kwa mujibu wa takwimu za TRA tayari tani 39,218 za mahindi zimeshauzwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Bodi ya Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na Soko la Bidhaa, imeendelea kuhamasisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutumika katika mazao ya kilimo ikiwemo mahindi na mpunga ili kuyafikia masoko ya ndani na nje ya nchi. Vilevile Wizara imeendelea kuhamasisha sekta binafsi kujenga viwanda ili kupata soko la uhakika la mazao ya kilimo. Viwanda vimeendelea kuongezeka vikiwemo vya EPZA, kufufuliwa kwa vinu vya nafaka vya Iringa, Arusha, Mwanza na Dodoma chini ya Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko na kile cja Mlali - JKT kilichozinduliwa tarehe 8 Aprili, 2019 na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na vingine vingi vinavyoendelea kuanzishwa na wafanyabiashara wadogo na wakubwa nchini.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itasimamia na kuhakikisha Madereva wa Malori na Mabasi wanapata Mikataba ya Ajira ili kuboresha maslahi yao na kuongeza ufanisi katika Utumishi wao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kushughulikia haki na maslahi ya Madereva nchini Tanzania, Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kutatua changamoto zinazowakabili madereva ambapo mnamo tarehe 2 Mei, 2015 Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliagiza iundwe Kamati ya Kudumu ya Kutatua Matatizo katika Sekta ya Usafirishaji chini ya Uenyekiti wa Katibu Mkuu wa iliyokuwa Wizara ya Uchukuzi. Aidha, Kamati ndogo chini wa Uenyekiti wa iliyokuwa Wizara ya Kazi na Ajira iliundwa kwa ajili ya kushughulikia haki, maslahi na mkataba wa ajira wa Madereva.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi Madereva na Viongozi wa Umoja wa Wamiliki wa Vyombo vya Usafirishaji nchini waliufanyia marekebisho na kuuboresha Mkataba wa ajira wa Madereva uliokuwepo. Mkataba ulioboreshwa uliidhinishwa na wadau katika kikao kilichofanyika tarehe 23 Juni, 2015 na ilikubalika kwamba Mkataba huo uanze kutumika rasmi tarehe Mosi, Julai, 2015.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, masharti yamewekwa kwamba kila Mmiliki wa basi au lori anayeomba leseni ya usafirishaji toka SUMATRA ni lazima awasilishe mikataba ya ajira ya Madereva wake ambayo imehakikiwa na Maafisa wa Kazi wa maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kusimamia majadiliano baina ya Vyama vya Wafanyakazi, Madereva na Umoja wa Wamiliki wa Vyombo vya Usafirishaji ili kuwawezesha kufikia muafaka wa viwango vya posho za safari na kujikimu wakati Madereva wanaposafiri ndani na nje ya nchi.