Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Oran Manase Njeza (72 total)

MHE. ORAN M. NJENZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, kwanza napenda kumshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na vilevile kuipongeza Wizara hii kwa kazi nzuri inayoifanya kwa kusambaza umeme karibu vijiji vyote vya Tanzania hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuwapongeza Mainjinia wa TANESCO waliopo pale Mbeya akiwemo Engineer Maze na Engineer Kiduko pamoja na Engineer Mbalamwezi. Pamoja na hayo, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Wizara ina mpango gani wa kusambaza umeme pamoja na hii REA kwenye vitongoji vilivyobaki katika vijiji hivyo vilivyotajwa? (Makofi)
Swali la pili, kutokana na ongezeko la usambazaji wa umeme vijijini, inaelekea capacity ya watumishi wa TANESCO ikiwemo vifaa, haitoshelezi tena.
Je, Wizara ina mkakati wa kuhakikisha kuwa inaongeza capacity ya watumishi ili iendane pamoja na usambazaji wa umeme vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika pamoja na Mheshimiwa Mbunge, ni kweli kabisa, pamoja na mradi huu kabambe wa REA kuendelea kufanya kazi yake, lakini bado kuna miradi mingine itaendelea kwa ajili ya kukamilisha shughuli zinazoachwa na REA. Baadhi ya kazi zinazoendelea hapa sambamba na miradi ya REA ni pamoja na mradi wa Underline. Mradi wa Underline unaendelea kupita kukamilisha maeneo ambayo yanaachwa na TANESCO pamoja na REA.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na uwezo na capacity pamoja na management, ni kweli kabisa, kama mnavyojua, TANESCO ni shirika la zamani, lakini tuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge pamoja Serikali ya Awamu ya Tano, ni kwamba tunapata uwezo wa kuongezewa nguvu. Kwa sasa hivi tunaongezewa nguvu Shirika letu la TANESCO kwa maana ya kulinunulia vifaa vya kutosha kama transfoma pamoja na generetors ambako tunatumia mafuta. Kwahiyo, Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie kwamba Shirika la TANESCO pamoja na REA pamoja na miradi mingine, itaendelea kuimarishwa ili ifanye kazi zake vizuri.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Mwenyekiti, na pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini nina maswali madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mradi wa haya madini adimu duniani pamoja na joto ardhi ni muhimu sana kwa uchumi wa viwanda, naomba commitment ya Serikali, moja, je, ni lini wataanza uchimbaji wa joto ardhi ili tuweze kutumia kwenye viwanda vyetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, na pili, naomba pia commitment ya Serikali pamoja na mradi wa Ziwa Ngozi, je, Serikali imetoa leseni ngapi za uchimbaji na uzalishaji wa madini na nishati ya joto ardhi katika sehemu zingine hapa kwetu Tanzania? Ahsante.
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya ni lini tunaanza, utafiti umeshafanyika, unaonesha kwamba ili upate umeme wa joto ardhi unahitaji kuwa na temperature ambayo iko katikati ya nyuzi 180 mpaka 240 celsius. Sasa bahati nzuri hii ya Ngozi iko zaidi ya 240. Kwa hiyo, kinachofuata sasa kwa miezi michache ni kwamba inabidi tuchoronge miamba pale chini tuweze kujua kuna mvuke kiasi gani ambao utaendesha mashine ya kuzalisha umeme wa kiasi gani. Kwa hiyo, tutatoa hiyo tarehe baada ya kujua tuna mvuke wa chini kiasi gani yaani steam.
Mheshimiwa MWenyekiti, na leseni ngapi zimetolewa, ni kwamba tumeshatengeneza ramani ya nchi nzima ambayo inaonesha maeneo yote ambayo tunaweza kuendeleza joto ardhi. Kwa sasa hivi ukiacha ya Ngozi, Mbeya eneo lingine ni la Luhoi kilometa kama 70 Kusini Mashariki mwa Dar es Salaam, halafu na lingine liko sehemu za Kusini mwa Morogoro na Ziwa Natroni kwa hiyo maeneo ni mengi lakini tunaenda hatua kwa hatua.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Kwa kuwa Waziri amepotoshwa kwenye jibu (b) sehemu ya kwanza ya swali langu na hivyo kuwapotosha wananchi wa Mji Mdogo wa Mbalizi na pia kulipotosha Bunge; je, Waziri atachukua hatua gani kwa Afisa huyo aliyempotosha?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ndani ya Mji Mdogo wa Mbalizi kuna ardhi ya zaidi ya ekari 5,000 iliyokuwa Tanganyika Packers, na haijaendelezwa kwa zaidi ya miaka 30 sasa na kwa kuwa Halmashauri ya Mbeya imetenga eneo mahsusi kwa kunenepesha mfugo na kwa ajili ya kiwanda cha nyama, je, ni lini Serikali itarudisha ardhi hiyo kwa Halmasahuri ya Mbeya kwa madhumuni ya makazi bora na huduma za jamii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Sasa naomba nitoe msisitizo katika eneo la kwanza ni kwamba Ofisi ya Rais - TAMISEMI tunapofanya hizi kazi tunahakikisha kwamba coordination inakamilika vizuri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge kama unaona kwamba kuna mapungufu, naomba u-clarify ni eneo gani ambalo linaonekana halijakuwa sawasawa, ili mimi kama Naibu Waziri, Ofisi ya Rais TAMISEMI nijue kwamba eneo gani ambalo halikukaa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la opotoshaji limekuwa la jumla, lakini hili tulilielekeza katika ofisi zote za mikoa, kwamba ma-RAS wote wako responsible katika majibu yote yanayojibiwa na TAMISEMI. Kwa hiyo, nilitaka angalau ungenipa ufafanuzi ni eneo gani uliona kwamba lilikuwa na mapungufu tuweze kulifanyia kazi kubwa, kwa sababu lengo kubwa ni kujenga, kwamba ni jinsi gani majibu yawe sawasawa kwa ajili ya kuboresha mahitaji ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika eneo la pili…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri amesema hivi swali lake kipengele (b) hakijajibiwa kabisa kwa maana hiyo, kwa sababu umepotoshwa majibu ya kipengele chote.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kuhusu swali la ni lini Serikali itarudisha eneo hili kwa ajili ya wananchi, mimi nilifika pale Mbeya nilipokwenda kutembelea Iyunga lakini nikafika katika Jimbo la Mheshimiwa. Mimi naipongeza Serikali kwa sababu kuna juhudi kubwa imefanyika, sasa pale kuna machinjio ya kisasa kwa ajili ya uchinjaji wa nyama tena wa kisasa katika eneo hilo la Mbeya. Lakini kwamba kuna eneo kubwa sasa eneo hili jinsi gani litafanyiwa kutwaliwa kurudishwa kwa wananchi kwa ajili ya makazi, nadhani sasa jambo hili ni jambo la mchakato, si jambo la kutoa maelekezo tu hapa, nini kifanyike haraka haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu lazima tufanye tathimini ni kitu gani kilichokuwepo hapo, kwa sababu inawezekana ukienda ndani kuna migogoro mingine ya ziada. Kwa hiyo, naomba niseme kwamba hilo ni suala zima la mchakato, naamini kwamba Baraza la Madiwani likikaa litafanya maamuzi litapeleka mapendekezo halafu vyombo husika vitakuja kufanya tathimini. Vitakaporidhika TAMISEMI - Ofisi ya Ardhi tutafanya tathimini ya kinakuona kama eneo hilo linaweza likarudishwa kwa ajili ya maslahi ya wananchi ili wananchi wapate huduma ambayo inahitajika katika maeneo yao.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na pia nashukuru kwa juhudi za misaada ya UNICEF kwa kuboresha elimu kwenye Halmashauri ya Mbeya na sehemu nyingine za nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi hizo, changamoto nyingi, hasa kwa shule za vijijini ni miundombinu. Ukichukulia mfano wa Jimbo langu la Mbeya Vijijini, Shule ya Msingi Ipwizi ya ina walimu wawili na wanafunzi wanaozidi 200; Shule za Iyanga, Shule za Ivwanga hazina hata mwalimu na hizo ziko karibu sana na Jiji la Mbeya.
Mheshimiwa Spika, shule nyingine kama za Kitusi na Ivwanga wanafunzi wanatembea zaidi ya kilometakumi kwenda Mkoa mpya wa Songwe kwa ajili ya kujipatia elimu.
Je, ni kwa nini misaada hii haijalenga kwenye changamoto muhimu za miundombinu katika shule zetu za vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kweli hili jambo analolisema Mheshimiwa Mbunge lipo na juzi tarehe tano tulipokuwa katika Mkutano wa Programu ya Walimu ya Mpango wa KKK pale Rungwe miongoni mwa changamoto ambayo niliiona ni kwamba kuna mshiriki mmoja alishindwa kuhudhuria mafunzo yale kwa sababu idadi ya walimu ni chache katika shule yao. Na ndiyo maana juzi tulikubaliana kwamba RAS Mkoa wa Mbeya anaweza kupitia michakato ya mgawanyo wa walimu katika shule zote kwa sababu imebainika kwamba kuna baadhi ya walimu wamelundikwa katika baadhi ya maeneo na maeneo mengine wamekosa walimu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa hili jambo unalosema sio jambo la uongo.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa Mkoa wa Mbeya jambo hilo lipo na RAS Mkoa wa Mbeya Mama yangu Mariam Mtunguja, amelibeba hili na tumekubaliana ndani ya mwezi huu atafanya reallocation vizuri ya walimu katika Mkoa wake wa Mbeya.
Mheshimiwa Spika, lakini suala zima la ajenda ya miundombinu ni kweli naomba tuendelee kushirikiana. Lakini wakati mwingine hii misaada inayotoka kwa wafadhili, inawezekana wao wana malengo yao maalum katika eneo lao.
Mheshimiwa Spika sisi kwanza tunapenda kuwashukuru sana wenzetu wa UNICEF kwa kazi kubwa wanayofanya, na tutajitahidi vile vile kuwashawishi wadau mbalimbali katika baadhi ya misaada, japokuwa itakuwa na capacity building, basi tutatafuta wengine ambao wataweza kutusaidia katika suala zima la infrastructure, jinsi gani tutawekeza miundombinu katika maeneo yetu, lengo kubwa ni kupunguza kero kwa wananchi wetu na hasa watoto wetu wanaotembea umbali mrefu.
MHE ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kwenye Mji mdogo wa Maswa tuna tatizo kama hilo kwa Mji wetu Mdogo wa Mbalizi, ambapo Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliahidi kumalizia kipande kidogo cha barabara ya kilometa moja na pia aliahidi kumalizia ujenzi wa stand pale Mbalizi lakini mpaka leo hakuna chochote kinachofanyika labda ningepena Waziri ajaribu kutoa ufafanuzi ni lini ujenzi huo utaanza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI YA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ujenzi kwanza naomba tukiri wazi kwamba bajeti katika kipindi ambacho Dkt. John Pombe Magufuli anaahidi bajeti yake ndio kwanza hii tunaanza bajeti ya kwanza na baadaye tuna miaka mitano. Lakini ameahidi stand na amewaahidi barabara ya kilomita moja. Mheshimiwa Mbunge, naomba nikwambie kwamba, ahadi ya Rais itakuwepo palepale na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu kazi hii na sisi tuliopewa dhamana ya kuisimamia, tutaisimamia kwa karibu zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaisimamia kwa karibu zaidi, lengo ni kwamba, ahadi ya Rais aliyoitoa, ujenzi wa stand, ujenzi wa barabara ya kilometa moja itafanyika na muweze kuona kwamba, maeneo mbalimbali sasa hivi stand zinajengwa kupitia miradi yetu sio stand tu, kuna ma-dampo, kuna barabara. Kwa hiyo, nikwambie Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, katika maeneo ya Mbalizi ni kwamba, watu wawe na subira hii ndio bajeti yetu ya kwanza imeanza. Imani yangu ni kwamba, maeneo ya Mbalizi, kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi, suala lile litatekelezwa.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Napenda na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza. Pamoja na Jimbo la Mbeya Vijijini kuwa na vyanzo vya uhakika wa maji kutoka Mlima Mbeya, lakini maji yamekuwa yakipelekwa Jijini Mbeya badala ya kupelekwa kwenye sehemu zenye uhaba mkubwa wa maji kwenye vijiji vya kata ya Mjele na Utengule Usongwe. Je, ni lini Wizara itapeleka maji safi kwenye vijiji vya kata za Mjele na Utengule Usongwe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru ameuliza swali zuri sana, ni swali la kisera. Nimhakikishie kwamba tayari tumeshatoa maelekezo eneo lolote ambalo chanzo cha maji kinaanzia pale, vijiji vilivyo karibu na chanzo ndiyo viwe vya kwanza kupata maji.
Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tunalielekeza kwa Wakurugenzi wa mamlaka ambao wanahusika na huo mradi, wahakikishe katika eneo hilo kwanza wanawapa maji wananchi waliopo pale baadaye sasa ndiyo wanapeleka maeneo mengine ya mjini. Kwa hili, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nitalifuatilia mimi mwenyewe.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kama ilivyo kwenye Jimbo la Busokelo kuna barabara ya Mbalizi kwenda Makongorosi ambayo inapitia kwenye Bonde la Ziwa Rukwa ambayo tumegundua neema ya gesi nyingi sana. Sasa ni lini Serikali itajenga barabara hiyo ya Mbalizi - Makongorosi kwa kiwango cha lami ambayo ni ya Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe? Ahsante.
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali tunaifahamu barabara hiyo na tuna mpango thabiti wa kuijenga. Lakini kwanza tupo katika mchakato wa awali hapo utakapo kamilika tutamtafuta mkandarasi ili tuweze kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. ORAN M. NJENZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, suala la Mji Mdogo wa Mbalizi kuna changamoto kubwa za maji kama iliyokuwa kwa Mji wa Mikumi. Je, ni lini mtatatua changamoto kubwa ya maji kwenye Mji Mdogo wa Mbalizi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya tuliwasiliana nae nikiwa kwenye ziara Mbeya na tukawa tumekubaliana kwamba tufanye mapendekezo, Wizara imeshaagiza tayari kwamba Mamlaka ya Maji ya Mkoa wa Mbeya ijipanue ili iweze kuhudumia mpaka eneo la Mbalizi. Tayari wanaendelea na utaratibu huo wameshafanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbalizi na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbalizi ameonekana kuridhia ili Mamlaka ya Maji ya Mbeya iweze kupeleka miundombinu mpaka Halmashauri ya Mbalizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niahidi kwamba taratibu hizi zitakamilishwa na wananchi wa Mbalizi watapata huduma ya maji kutokana na Mamlaka ya Maji ya Mji wa Mbeya.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupewa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo kwa mkutano tuliofanya na wakulima na wawakilishi wa Wanunuzi mwishoni mwa mwaka 2016.
Mheshimiwa Spika, katika mkutano huo tulikubaliana kuwa wanunuzi wadogo wapewe leseni ya muda na vile vile wajiunge kwenye vikundi na pia hii Kampuni ya pareto ambayo ilikuwa imebinafsishwa kutoka Serikalini kulikuwa na asilimia 10 ambazo walipewa wakulima. Vilevile katika hicho kikao tulikubaliana kuwa zichunguzwe hizo asilimia kumi ziko kwa nani kwa vile wakulima hawakupewa hizo asilimia kumi.
Mheshimiwa Spika, pamoja na makubaliano yote hayo, hakuna hata kimoja kilichozingatiwa na leo hii kuna kampuni mpya mbayo imejenga kiwanda eneo la Inyara, Mbeya ambayo imezingatia vigezo vyote na ilipewa leseni ya kununua pareto kwenye vijiji viwili tu kati ya vijiji zaidi ya 20 vinavyolima pareto. Sasa ni kwa nini Serikali isiboreshe hii Bodi ya Pareto ili tuweze kuboresha kiwango cha zao la pareto?
Mheshimiwa Spika, nashukuru.
La pili vilevile nilitaka kupata uhakika wa Serikali, kwa sababu inavyoelekea hakuna ushindani sasa hivi, watatuhakikishia vipi ya kwamba hawa ambao wametimiza vigezo vyote wanaruhusiwa kununua pareto ili inunuliwe kwa ushindani? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba Mheshimiwa Njeza amekuwa akifuatilia sana maslahi ya wakulima wake wa pareto, kahawa na mahindi. Kwa hiyo, tumekuwa naye karibu sana. Vilevile nikiri kwamba tulifanya kikao na wakulima, mkutano ambao ulitusaidia sana kupata makubaliano kuhusu namna bora ya kuendesha zao la pareto.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mazungumzo yetu, baadhi ya masharti ambayo wakulima na wawakilishi wao tulikubaliana watekeleze, bado wako mbioni kutekeleza na hivyo bado tunasubiri kutoka kwao.
Mheshimiwa Spika, vile vile kuhusiana na leseni ya kampuni za kununua pareto; nilieleze tu Bunge lako Tukufu kwamba zao la pareto ni zao lenye masharti tofauti kidogo na mazao mengine kwa sababu tunachoruhusu kipelekwe nje siyo pareto ghafi, siyo maua, bali ni sumu ghafi. Katika maana hiyo, ili uweze kupeleka nje lile zao ni lazima uwe na kiwanda.
Mheshimiwa Spika, tunafanya hivyo kwa sababu huko nyuma wakati tulikuwa tunaruhusu kupeleka maua nje, kiwango cha pareto yetu kilishuka sana kwa sababu hatukuwa tunaweza kudhibiti ubora wa sumu inayopelekwa nje, ndiyo maana tukaleta ili kunusuru zao lisije likaanguka nchini. Tukaleta kigezo kwamba ni lazima uweze kuwa na kiwanda ili uweze kuzidua au kuchakata na kuwa sumu ghafi.
Kwa hiyo, kampuni yoyote ambayo imekidhi masharti hayo, katika hali ya kawaida tunaruhusu inunue pareto. Kampuni ambayo anaizungumzia ya TAN Extract ya Mbeya ambayo ndiyo imeingia tu sokoni na kutimiza masharti, tutaendelea kutoa leseni ili waweze kununua pareto maeneo mengine zaidi ya vijiji ambavyo wanatoa sasa.
Vilevile nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa hatujaona kwamba tatizo ni Bodi ya Pareto lakini ni kanuni na sheria ambayo tumewekeana wenyewe kama wadau na Serikali iko tayari kuirejea na kuangalia upya sheria na kanuni hizo kama itaonekana inafaa.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kama ilivyo kwa Jimbo la Kwela, kuna barabara mbili ambazo ziliahidiwa na Mheshimiwa Rais; Barabara ya Mbalizi kwenda Makongorosi ambayo inaunganisha Mbeya na Mkoa mpya wa Songwe. Pia kuna barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete mpaka Njombe ambayo vile vile inaunganisha Mikoa ya Mbeya na Njombe ziliahidiwa na Rais kwamba zitajengwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini hizi barabara zitajengwa kwa kiwango cha lami pamoja na kulipa fidia wale wote ambao ni waathirika.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba serikali imeshaanza kuchukua hatua za dhati kabisa za kujenga barabara ya kutoka Isyonje – Makete na hiyo barabara yote tumeshaanza hatua na kwamba wakandarasi wameshatafutwa na nadhani anafahamu Mheshimiwa Mbunge na hasa nikijua amemuulizia vile vile Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Miundombinu ambaye naye yupo katika barabara hiyo. Nimhakikishie Serikali itatekeleza kile ambacho imekusudia na imeanza kukitekeleza.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa ajili ya matatizo ya migogoro ya wafugaji na wakulima, maeneo mengi yanahitaji sasa hivi kuwe na vituo vidogo vya Polisi. Je, Serikali au Wizara inatupa commitment gani kuwa kutakuwa na vituo vya Polisi katika maeneo hayo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wananchi wamekuwa wakijitolea kujenga vituo vya Polisi kama ilivyokuwa kwa kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mbeya ambao wamejenga kwa asilimia karibu zaidi ya 50. Je, Serikali inawaahidi nini wale wananchi wa Mbalizi kuwaunga mkono kuwamalizia kile kituo chao cha Polisi? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpe pole Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete kwa kupatwa na msiba na ndiyo maana hajaweza kuwepo kuuliza swali. Mungu ampe moyo wa ustahimilivu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la nyongeza alilouliza Mheshimiwa Oran; moja kituo cha Mbeya ambacho wameshafanya kazi kubwa sana nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amefanya hamasa kubwa sana na najivunia kwamba nilikwenda kumuunga mkono wakati wa kampeni. Kwa kuwa amefanya kazi kubwa sana na sisi kama Wizara tuna bajeti ambayo tumetenga kwa ajili ya umaliziaji wa majengo ambayo yameshafikia hatua kubwa. Hivyo, tutafanya ziara, tutajionea na tutaweka wataalam ili waweze kukadiria na kwenda kwenye utekelezaji wa umaliziaji ili nguvu ya wananchi isiweze kupotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa vituo karibu na maeneo ambayo yanakuwa na migogoro ya mara kwa mara, Serikali inaendelea kufanya utaratibu wa kuweza kuwepo vituo hivyo lakini pale ambapo vituo hivyo havipo tutaendelea kufanya doria ili kuweza kuhakikisha kwamba tunawahakikishia wananchi usalama wao punde panapokuwepo na migongano ya aina hiyo hata kama bado hatujaweka vituo vya Polisi.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuna shule Shikizi nyingi ambazo zina Walimu wa kujitolea na hawapati posho. Je, ni lini Serikali itaanza kuwalipa posho hawa Walimu wanaofundisha kwenye Shule Shikizi? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, katika jambo hili nadhani kila Halmashauri ina mkakati wake ku-address matatizo ya watumishi katika maeneo mbalimbali; na kuna baadhi ya maeneo mengine utakuta watu wanatumia own source kuonesha jinsi gani wana-address hili jambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kuna mambo specific katika eneo la Mheshimiwa Njeza, tutalichukua halafu tuangalie jinsi gani tutafanya kuona nini kimetokea huko ilimradi tuliweke sawa ili kila mtu apate stahiki yake. Kama kuna maeneo mahususi katika Halmashauri husika, basi tutayatoa kwa lengo la kuweka mustakabali mzuri katika maeneo yetu hayo.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata tafsiri ya jina langu.
Mheshimiwa Spika, kwa kweli nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali yanayotia moyo, pamoja na kuwepo na jitihada za kuweka mfumo mzuri wa masoko, bado mfumo wa masoko umedhoofishwa na kuwepo kwa wanunuzi wachache ambao wamekuwa wakiwadidimiza wakulima kwa bei isiyokuwa ya ushindani.
Swali la kwanza, je, ni kwa nini zao la pareto lina mnunuzi mmoja ambaye anajipangia bei anavyotaka mwenyewe?
Swali la pili, je, ni kwa nini tumeshindwa kuanzisha soko la bidhaa (commodity exchange) ambayo imekuwepo toka mwaka 2014?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, kwa nini soko la pareto lina mnunuzi mmoja. Naomba nimueleze Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kipindi kirefu pareto imekuwa inanunuliwa na mtu kwa sababu masharti yaliyopo katika ununuzi wa zao la pareto ni kwamba ni lazima mnunuzi awe na kiwanda kwa sababu kinachouzwa kwenye pareto siyo maua ni ile sumu. Sasa kama hatujui kiwango cha sumu kilichopo kwenye maua ni vigumu sisi kujua bei ambayo wakulima wetu wanapata vilevile ni vigumu hata kukokotoa kodi ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, naomba nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa kuna kiwanda cha pili kimejengwa Mbeya, kwa hiyo tunaamini kwamba kitaongeza ushindani. Nafahamu ameshaniletea malalamiko mara nyingi sana kwamba pamoja na kuja na hichi kiwanda bado kuna vizingiti vya kuhakikisha kwamba kiwanda cha pili nacho kinaruhusiwa kununua pareto, naomba tu nimhakikishie yeye pamoja na wakulima wake kwamba mimi mwenye nitafuatilia kuhakikisha kwamba huyu mnunuzi mpya aliyeingia sokoni anaruhusiwa kununua bila vizingiti vyovyote.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la pili la commodity exchange. Ni kweli kwamba kwa muda sasa Serikali imekuwa ikifikiria kuanzisha mfumo wa commodity exchange kama namna mojawapo ya kutafuta masoko kwa ajili ya mazao yetu. Ili tuweze kuanzisha mfumo wa commodity exchange ambayo kimsingi ni mfumo wa kisasa zaidi wa stakabadhi ghalani unaotumia teknolojia kubwa zaidi na unaoweza kuunganisha mazao yetu katika soko la dunia tunahitaji vitu vingi sana ikiwa ni pamoja na teknolojia yenyewe ni lazima tuwe na maghala ambayo yanakidhi sifa za Kimataifa, vilevile lazima tuweze kufanya na uzalishaji ule wa bidhaa ambao unapatikana kwa quality ile ambayo inahitajika na kwa viwango ambavyo soko la dunia linahitaji.
Kwa hiyo, tunafikiri kwamba wakati tunaendelea kuboresha mazingira yetu ya ndani tutaendelea kwa sasa kutumia utaratibu wa stakabadhi ghalani na tumeona mafanikio makubwa sana kwenye korosho na tayari tunaelekea kutaka kuuza mazao mengine kama mbaazi, ufuta kwa kutumia utaratibu huo. Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hatujalitupa lakini bado tunaboresha mazingira ili iweze kufanikiwa kwa urahisi zaidi.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana vilevile nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kazi zilizokuwa zinaendelea zilizokuwa zinafanywa na Halmashauri na hizo zimehamishiwa kwenye TARURA sasa hivi. Je, ni lini TARURA wataanza na kuendeleza hizo kazi?
Swali la pili, kama ilivyo katika Mji Mdogo wa Rujewa vilevile Mheshimiwa Rais aliahidi kumalizia ujenzi wa kituo cha mabasi cha Mbalizi katika Mji Mdogo wa Mbalizi.
Je, ni lini kazi hiyo ya kujenga kituo cha mabasi cha Mji Mdogo wa Mbalizi kitaanza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tumekuwa na kipindi cha mpito ambapo kazi za ujenzi wa barabara katika Halmashauri zilikuwa zikisimamiwa ndani ya Halmashauri zetu, lakini chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Sasa hivi tumeunda Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ambao unaitwa TARURA sasa umeshaanza kuchukua majukumu hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tunafahamu wazi kwamba kulikuwa na mikataba mingine na kazi mbalimbali zilikuwa zinaendelea na tulitoa maelekezo katika ofisi yetu kwamba zile kazi zote kutokana na mikataba iliyokuwa inaendelea ambazo ziliingiliwa na Halmashauri kazi zile zilipaswa kuendelea, isipokuwa taratibu za malipo ndio zilikuwa zinafanyiwa utaratibu maalum. Tulitoa maelekezo haya kwa Mameneja wa TARURA katika nchi nzima katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hata hivyo, wakati mwingine kulikuwa na uelewa tofauti katika baadhi ya maeneo, baadhi ya maeneo kazi zilikuwa zinaendelea vizuri lakini sehemu zingine kazi zilisimama, kazi kubwa iliyofanyika ni kuhamisha zile akaunti ziweze kufanya kazi vizuri ili utaratibu uendelee kufanyika kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na concern yako Mheshimiwa Oran naomba niiagize Halmashauri yako Meneja kama kuna changamoto ambayo ameipata katika ofisi yake tuwasiliane na ofisi na hasa na Mtendaji Mkuu wa TARURA ampe maelekezo ya kutosha nini kifanyike, ili kazi kule site isiendelee kukwama, ziendelee kufanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la ujenzi wa stendi hii ya Mbarali, naomba nilichukue hili halafu nijue kwamba kuna kitu gani kilichokubaliwa na imefikia hatua gani? Changamoto iko wapi? Hili naomba niwahakikishie ofisi yangu itasimamia kwa sababu ahadi ya Mheshimiwa Rais lazima itekelezwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilichukue jambo hili tutaenda kulifanyia kazi haraka iwezekanavyo, kuangalia nini tufanye ili kuhakikisha ile stendi inatengenezwa.(Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nianze kwa kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kufanya ziara katika Halmashauri ya Mbeya na katika ziara yake tuliahidi kuwa mradi wa Iwindi wananchi wangeanza kupata maji kabla ya Desemba mwaka 2017, je, ni lini mradi wa maji kwa Vijiji vya Izumbwe, Iwindi, Mwashiwawala na Mbalizi utakamilika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Mbalizi, Mzee Njeza kwa kazi kubwa anayoifanya katika suala zima la kuhakikisha wananchi wake wanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa nilishafanya ziara kule lakini ipo changamoto baadhi yetu wataalam kushindwa kusimamia miradi. Moja, nataka nimhakikishie tu, katika hali niliyoiona nipo tayari kushirikiana naye lakini pia na watalaam wetu kwenda katika kusukuma miradi ile ili wananchi wake waweze kupata maji kwa wakati. Ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJENZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, napenda vile vile kushukuru majibu ya Serikali na pia nipende kutambua jitihada zinazofanywa na Serikali ya mkoa na TANAPA vile vile kwa kushiriki katika ujenzi wa kituo cha afya pale Ilungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza kwa vile hii fidia ni ya muda mrefu 1965; je, Serikali inathibitisha kuwa hii fidia itakayolipwa mwaka huu itazingatia thamani na sheria zilizopo sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa vile Mji wa Mdogo wa Igoma unakua kwa haraka sana na pale kuna eneo la hifadhi ambalo limezungukwa na mji; je, Serikali itakuwa tayari kuliachia lile ili liweze kutumiwa na shule pamoja na huduma zingine za kijamii? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu hilo swali, kwanza naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akifanya katika kufuatilia fidia hii ya wananchi wake na amefuatilia kwa muda mrefu na taarifa ziko nyingi sana na wananchi wajue kwamba Mheshimiwa Mbunge anafanya kazi nzuri sana hongera sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fidia, kama nilivyosema kwenye swali la msingi tunafanya tathimini upya mwezi Februari mwaka huu. Kwa hiyo, baada ya tathimini hiyo ni wazi kabisa kwamba tutabaini kwamba mahitaji au fidia inayotakiwa italingana na hali halisi ya leo na si ya mwaka 1965. Kwa hiyo wananchi watapata nafasi nzuri kabisa ya kupata fidia inayostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maombi yanayohusu hapa kujenga makao makuu kutokana na ongezeko la watu. Naomba nitoe maelezo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza maeneo mengi yameleta maombi ya namna hiyo yanayofanana, lakini hili ombi ambalo amelileta Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie tu nitachukua jukumu la kwenda kwanza kukutana na wananchi wenyewe ili niangalie hilo eneo kama kweli linafaa kutolewa kwa ajili ya huduma za jamii. Hata hivyo, mkazo zaidi utaendelea kusisitizwa kwamba hifadhi ni muhimu kuliko vitu vingine vyote.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Pamoja na Jimbo la Mbeya Vijijini kuzungukwa na milima inayotiririsha maji mwaka mzima, lakini wananchi katika vijiji vingi hawana maji salama.
Je, ni lini Serikali itajenga miundombinu kwa kuwapatia maji salama wananchi wa vijiji vya Mbeya Vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tunaendelea na usanifu na baadhi tumeshasaini mikataba kwenye Jimbo lake kuhakikisha kwamba wananchi wote wa Mbeya Vijijini, Jimbo la Mheshimiwa Mbunge wanapata maji safi na salama. Tulikuwa tumebuni miradi kwenye vijiji kadhaa lakini baadae tukagundua kwamba yale maji yatakwenda kwenye kijiji cha mwisho na kuacha vijiji vya katikati, tumechelewa kwa sababu ya kuhakikisha kwamba tunaainisha na vijiji vya katikati. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mwaka ujao wa fedha mapema kabisa tutasaini mikataba, na mimi Mheshimiwa Waziri ameshanipangia ratiba, katika ratiba Mikoa nitakayoizungukia ni pamoja na Mkoa wa Mbeya. Kwa hiyo ntahakikisha tunaambatana na wewe kwenda kwako ili tuweze kuona hivyo vijiji vyenye uhaba mkubwa wa maji.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nashukuru. Katika milima ya Panda Hill Wilaya ya Mbeya kuna madini ya niobium ambayo yanatarajiwa kuchimbwa hivi karibuni. Je, Serikali imechukua hatua gani na tahadhari gani ili yasije yakatokea yale yaliyotokea kwenye Acacia na Barrick Gold Cooperation?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana, Mgodi wa Niobium hapa Tanzania ni mgodi pekee ambao unapatikana katika eneo la Songwe. Kinachofanyika sasa ni majadiliano kati ya Magereza ambako eneo la mgodi litachukua ili kuona kama kutakuwa na re-settlement na majadiliano kama yakikamilika.
Kwa hiyo, nimpe taarifa tu, taratibu zinazofanyika sasa ni majadiliano kati ya Kampuni pamoja na Magereza, taratibu zikishakamilika basi uwekezaji utaendelea.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuna shule Shikizi nyingi ambazo zina Walimu wa kujitolea na hawapati posho. Je, ni lini Serikali itaanza kuwalipa posho hawa Walimu wanaofundisha kwenye Shule Shikizi? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, katika jambo hili nadhani kila Halmashauri ina mkakati wake ku-address matatizo ya watumishi katika maeneo mbalimbali; na kuna baadhi ya maeneo mengine utakuta watu wanatumia own source kuonesha jinsi gani wana-address hili jambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kuna mambo specific katika eneo la Mheshimiwa Njeza, tutalichukua halafu tuangalie jinsi gani tutafanya kuona nini kimetokea huko ilimradi tuliweke sawa ili kila mtu apate stahiki yake. Kama kuna maeneo mahususi katika Halmashauri husika, basi tutayatoa kwa lengo la kuweka mustakabali mzuri katika maeneo yetu hayo.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Wizara. Nikiri kweli kuwa wamefanya kazi nzuri ila katika haya majibu kuna Kijiji cha Mbuyuni bado hakijapata umeme pamoja na kuwa kimeorodheshwa kuwa kimo kwenye orodha ya vilivyopatiwa umeme.
Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ni umeme uliokwenda Idunde umeruka Vijiji vya Rukwa na Kapalala; Je, ni lini Serikali itahakikisha hivi vijiji vilivyobaki vya Kapalala, Mbuyuni na Rukwa vitapatiwa umeme ikiwa ni pamoja na vijiji vya Kata ya Ikukwa ambayo ni karibu sana na Jimbo la Songwe navyo vitapatiwa umeme?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, nakiri kuwa Serikali imefanya kazi nzuri ya kupeleka umeme vijijini, lakini kwa mazingira ya vijijini wanahitaji vilevile huduma kutoka TANESCO; Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuwa kutakuwa na huduma kwa wateja ambazo zitakuwa karibu huko vijijini ili waweze kupata huduma pamoja na hii huduma nzuri iliyofanyika kwa mpango wa REA? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na namshukuru sana Mheshimiwa Njeza kwa maswali yake mawili ya nyongeza. Nampongeza pia kwa kazi nzuri kwenye Jimbo lake.
Mheshimiwa Spika, katika maswali yake la kwanza amejielekeza kwenye Kijiji cha Mbuyuni ambacho anasema kiko kwenye orodha ya vijiji vyenye umeme, lakini pia hakina umeme. Naomba hili nilichukue ili tuweze kufuatilia takwimu hii na nitampa majibu ya uhakika.
Mheshimiwa Spika, pia, katika swali lake hilo alielekeza vijiji ambavyo vimerukwa ikiwemo vijiji vya Kata ya Ikukwe. Naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi vijiji vyote vilivyosalia 7,873 nchi nzima vitapata miundombinu ya umeme kwa mizunguko. Mzunguko wa kwanza na mzunguko wa pili.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, vile 3,559 vya mzunguko wa kwanza kazi inaendelea mpaka Julai, 2019 kisha tunaanza mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili. Kwa hiyo naomba nimthibitishe Mbunge maeneo ambayo yaliyosalia yatapatiwa miundombinu ya umeme kupitia REA awamu ya tatu mzunguko wa pili.
Mheshimiwa Spika, ameuliza suala la namna gani wananchi wa maeneo ya vijijini watapata huduma ya TANESCO. Naomba nilithibitishie Bunge lako Tukufu kuwa, kazi ya kupeleka miundombinu ya umeme inahusu vijiji vyote na tunatambua baadhi ya vijiji viko mbali na ofisi zetu za TANESCO ambazo ziko kila Wilaya, tumeielekeza TANESCO kufungua ofisi ndogo ndogo kwenye miji mikubwa na miji ambayo iko karibu na maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuthibitishie hilo linafanyika na tumeshapokea orodha ya ofisi za TANESCO ndogondogo mpya ambazo zingine zitajengwa lakini pia tumeomba pale ambapo, maana yake ujenzi ni suala la muda mrefu, lakini pale ambapo kuna maeneo ya vijiji kwenye Kata kuna Ofisi za Watendaji wa Kata, basi kipindi ambacho wataanza kuunganisha wateja tumeomba TANESCO waende kutumia hizo ofisi kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi wetu na nia ni kurahisisha utoaji wa huduma hizi kwa wananchi wa vijijini. Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, nina imani wahanga wengi akiwemo ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa atakuwa amefurahishwa sana na majibu haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bandari yetu ya Dar es Salaam ina ushindani mkubwa sana kutoka Bandari za Angola, South Africa pamoja na Msumbiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini Serikali itajenga Bandari ya Inyara ikiwa ni pamoja na reli ya kutoka Mbeya kwenda Ziwa Nyasa ili kukabiliana na ushindani huu wa kibiashara ambao ni karibu asilimia 70 ya biashara ya nje kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwa mizigo inayokwenda nchi za nje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi - Shigamba - Isongole na barabara ya Mbalizi - Makongorosi ambazo ni barabara za kimkakati na ilikuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne na Rais wetu wa Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niruhusu nimpe pongezi nyingi Mheshimiwa Mbunge Oran kwa kufuatilia mambo mbalimbali kwa sababu nafahamu anafuatilia masuala ya barabara, Uwanja wa Ndege wa Songwe, bandari kavu kama alivyouliza, lakini mambo muhimu kama ya kilimo na wachimbaji wake wadogo wadogo na mara nyingi tunapokea ushauri wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujibu swali lake la kwanza kuhusu ujenzi wa bandari kavu hususan eneo la Inyara, niseme tu kwamba Serikali inafanya maandalizi muhimu kwa ajili ya ujenzi wa hii bandari kavu ikiwa ni pamoja na kutenga eneo la heka 108 kwa ajili ya ujenzi huo. Eneo hili tumelitazama kimkakati kwa kweli kwa maana ya kuangalia ile chain supply yaani kuwa na mnyororo wa muunganiko kwa maana kwamba eneo hili linapakana na barabara inayotoka Mbeya au Kyela kwenda Malawi pia iko kandokando ya reli ya TAZARA.
Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tumejipanga kwa ajili ya kuboresha bandari hii na hatua ambayo tuko nayo ni kufanya tathmini ya maeneo ya wakazi wanaopitiwa na mradi huu ili tuweze kuwalipa fidia na harakati zingine zitakazofuata kwa ajili ya ujenzi wa bandari hii kavu ziwezi kuendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu barabara ya Mbalizi - Shigamba na barabara ya Mbalizi - Makongorosi ni barabara ambazo tumezizingatia pia katika bajeti yetu hii kwa maana ya kuziboresha. Mheshimiwa Mbunge anatambua kwamba tumetenga fedha nyingi kuboresha barabara hizi ili ziendelee kupitika wakati wote, wakati tunazitazama kwa ajili ya kuziboresha kwa kiwango cha lami.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba niiulize Serikali ni lini itapeleka maji kwenye Kata ya Mjele ambayo ni ahadi ya muda mrefu ya Serikali? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitumie nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya na nimeshafika hadi Mjele. Namwomba sana Mhandisi wa Maji wa Jimbo la Mbeya Vijijini asilale ili kuhakikisha wananchi wale wanapata maji safi, salama na ya kuwatosheleza. Jambo la msingi sisi kama Wizara a-raise certificate tuko tayari kulipa kwa wakati ili wananchi waweze kupata maji.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na vilevile nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kutokana na ajali nyingi zinazotokea katika Wilaya ya Mbeya na hasa katika Milima ya Uyole na Mbalizi. Je, ni lini Serikali itafanya upanuzi wa barabara zinazoelekea kwenye nchi za jirani za Zambia na Malawi?
Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itajenga by pass ya Inyala – Simambwe na Inyala – Songwe? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza niseme kwamba study zilizofanyika zinaonyesha kuwa ajali nyingi zinazotokea asilimia 78 zinatokana na makosa ya kibinadamu (human behavior) na asilimia 12 iliyobaki ndiyo inasababishwa na mambo mengine ikiwepo miundombinu. Kwa ajali ambazo zinatokea katika Mkoa wa Mbeya niseme tu ajali iliyotokea juzi kwa mfano nimepata fursa ya kuwepo Mbeya juzi, eneo ajali ilipotokea ni eneo ambalo barabara ni nzuri na alama za barabarani zipo, inawezekana lilikuwa tatizo la kiufundi lakini tu kwa ujumla wake Serikali imechukua hatua ya kuendelea kuboresha barabara za Mbeya kwa sababu nature ya eneo la Mbeya ni milima na miteremko mirefu ili kuweza kupunguza ajali kwa maana kwamba ile barabara sasa anayoitaja Mheshimiwa Mbunge Inyala – Simambwe ni kati ya barabara ambazo tunaendelea kufanya usanifu ili tuweze kupunguza ule msongamano mkubwa wa magari.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa ujumla wake tu ninapende kutoa wito kwa watumiaji wa barabara kwamba maeneo haya ambayo yanakuwa na milima mikali na alama za barabarani zipo, watumiaji wa magari tuzingatie hizo kanuni za barabarani ili tupunguze ajali wakati Serikali inafanya juhudi za kuboresha barabara zake. Kwa hiyo, tatizo la Mbeya niseme kwa ujumla Serikali inalitambua na tunafanya haraka kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu na kupunguza ajali katika eneo hili.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, na ni nia ya wananchi kuona kuwa eneo hilo linatengwa na kunakuwepo na viwanda ili wananchi wa Mbeya waweze kupata ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo mikakati mizuri, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Je, ni lini sasa Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kumalizia Kiwanda cha Kuchakata Nyama ambacho kimejengwa na Halmashauri ya Mbeya na ambacho vyombo vyote, vifaa vyote zaidi ya miaka miwili sasa viko mle ndani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa vile kuna wafugaji wengi katika Kata ya Mjele na tatizo lao kubwa ni mabwawa ya maji, je, ni lini Serikali sasa itapeleka miundombinu ya mabwawa ya maji kwa ajili ya mifugo na binadamu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwamba amekubaliana na majibu ya Serikali kwenye swali la msingi na katika maswali yake mawili ya nyongeza, la kwanza, kuhusu mradi wa kiwanda cha kusindika nyama pale Mbalizi ambao uliwasilishwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Vijijini TAMISEMI kwa ajili ya kufikiriwa kupewa fedha ni miongoni mwa miradi ya kimkakati katika halmashauri hiyo ambayo imeombewa fedha kwenye dirisha maalum la miradi ambayo ni miradi ya kibiashara.
Kwa hiyo, mchakato wake bado unaendelea, kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha miradi hiyo yote bado inafanyiwa upembuzi maalum ili utakapokamilika miradi ile ambayo itapatiwa fedha wahusika wa Halmashauri wataarifiwa. Hata hivyo ninaamini mradi huo ni mzuri na una faida na miradi kama hiyo Mbeya haipo mingi, kwa hiyo, ninaamini utapewa kipaumbele unaostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu bwawa kwenye eneo la wafugaji. Najua Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi alitembelea eneo hilo na akatoa ahadi. Mimi nataka nimwambie kwamba Serikali hii ni moja, nitafuatilia mimi mwenyewe kwa Wizara ya Mifugo ili kuhakikisha kwamba Halmashauri na wakazi wa eneo hilo wafugaji wanapata kile ambacho Mheshimiwa Naibu Waziri alikiahidi. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Swali langu, je, ni lini Serikali itaamisha gereza la Songwe ili kupisha mradi wa mgodi wa niobium ambao una thamani ya zaidi ya dola bilioni 6.8 ambayo ni sawa na shilingi bilioni 15. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lake linauliza ni lini, nadhani sitaweza kujibu kwa lini sasa hivi hapa kabla ya kuweza kulifanyia utafiti. Ningeomba anipatie muda nilifanyie utafiti jambo lake hili nijue hasa undani wa hili tatizo lake lilivyo ili niweze baadaye kukaa nizungumze naye pembeni kuweza kumfahamisha kama ni lini litahamishwa au kama kuna mipango mingine ambayo ipo ya kuweza kukabiliana na tatizo ambazo amelizungumza.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwanza nianze kabisa kuipongeza Serikali pamoja na changamoto zote hizi za miundombinu na idadi ndogo ya askari lakini bado wameimarisha ulinzi katika Wilaya ya Mbeya na hususani Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi.
Swali la kwanza, je, ni lini Serikali itapeleka shilingi milioni 120 ambazo zitaunga mkono shilingi milioni 200 walizotumia wananchi kukamilisha Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi?
Swali la pili; je, ni lini Serikali itajenga Vituo vya Polisi katika miji inayochipukia ya Mjele, Ilembo pamoja na Igoma? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika umaliziaji pamoja na majengo mapya aliyoyasemea tutaweka kipaumbele katika mwaka huu wa fedha pamoja na bajeti zitakazofuatia kulingana na upatikanaji wa rasilimali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze tu Mheshimiwa Mbunge, amefanya jitihada kubwa sana katika jengo hili ambalo tunalisemea na aendelee na moyo huo huo na ndiyo maana wananchi wa Mbalizi pamoja na Mbeya Vijijini wanaendelea kumuamini na kuchangua.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri kwa ziara walizozifanya kwenye Halmashauri ya Mbeya. Naibu Waziri alitembelea kata ambazo hazina umeme kabisa lakini zinalizunguka Jiji la Mbeya kama Kata za Swaya na Maendeleo. Je, ni lini hizi kata mbili nazo zitapewa umuhimu wa kupewa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tukushukuru sana kwa namna ambavyo umetambua mahitaji ya nishati na kuwapa fursa Waheshimiwa Wabunge kuuliza maswali mengi. Umenipa fursa ya kujibu maswali ya Mheshimiwa Njeza, Mheshimiwa Mwamoto pamoja na Mheshimiwa Frank.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Njeza na Mheshimiwa Mwamoto maswali yao yanalingana kwa sababu yamehusisha masuala ya umeme vijijini. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Njeza, tulifanya ziara Mbeya, pamoja na kwamba Jimbo lake ni Mbeya Vijijini, hapa amezisemea kata ambazo zipo ndani ya Jiji la Mbeya, na kama nilivyosema, Serikali imetambua ukuaji wa maeneo katika Miji, Manispaa na Majiji na ndiyo maana tumekuja na mradi huu unaoitwa Peri-Urban. Niliombe Bunge lako tukufu, tutakapowasilisha bajeti yetu ya mwaka 2018/2019 ituunge mkono katika miradi mbalimbali ukiwemo Mradi huu wa Peri- Urban kuupitisha kwa kishindo kisha tufanye kazi ya kupeleka umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa na huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, Mheshimiwa Mwamoto, ni kweli tulifanya ziara tena kwa mara ya kwanza Mawaziri wawili, Mheshimiwa Waziri mwenyewe na mimi Naibu Waziri tulikuwa kwenye kata hiyo aliyoitaja. Nataka niseme sisi lengo letu ni kupeleka nishati kwenye maeneo yenye uhitaji ikiwemo mojawapo ya maeneo ambayo kweli yanahitaji nishati ni eneo la viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwapongeze Mheshimiwa Mbunge na vijana hao kwa kutenga eneo la viwanda vidogo vidogo na kwa gharama za Serikali umeme utafika katika maeneo hayo na nitoe rai tu wao waendelee kujipanga kuunganisha lakini umeme utafika kama ambavyo tumeahidi katika ule mkutano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la mwisho la Mheshimiwa Frank, ni kweli Mji wa Tunduma ni mji ambao umekuwa na upo mpakani. Nataka niseme Mji wa Tunduma upo katika Mkoa mpya wa Songwe na wakati huo umeme katika Mkoa wa Songwe ulikuwa unatoka katika njia ya kusafirisha umeme ni ndefu kutoka Mbeya. Serikali ina mpango wa kujenga sub-station palepale Tunduma kwa ajili ya kuufanya Mkoa mzima wa Songwe upate nishati ya uhakika na wakati wote. Kwa hiyo, nimthibitishe Mjumbe kwa kuwa yeye Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Kamati yetu ya Nishati na yeye pia atuunge mkono katika bajeti yetu ili mradi huu wa ujenzi wa sub-station pamoja na line ambayo inatoka Mbeya inayoenda Sumbawanga - Mpanda – Kigoma - Nyakanazi ya KV 400 ambayo yote kwa pamoja itachangia kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika. Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niulize swali dogo tu, ni lini ujenzi wa Bandari Kavu utaanza ya Mbeya ambayo ni ya kimkakati kwa ajili ya kuhudumia mizigo ya nchi jirani za Zambia, Malawi na DRC? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tunalo eneo ambalo tumelichukua kupitia Mamlaka ya Bandari Tanzania kwa ajili ya kuweka Bandari Kavu katika Mkoa wa Mbeya. Sasa hivi utaratibu unaoendelea ni kuhakikisha tunalipa fidia kwa wananchi kwa eneo lile ambalo kwa kweli nikiri kwamba ni la kimkakati kwa ajili ya kuhudumia mizigo ya Zambia, Malawi na hata DRC. Tukishamaliza mchakato wa kulipa fidia kwa wananchi, tutaweka mipaka na kutengeneza ramani kwa ajili ya kutengeneza bandari hiyo kavu ili iweze kutoa huduma hizo.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, nashukuru pia kwa majibu ya Serikali hasa kwa kutambua kuwa hizi ni barabara muhimu za kimkakati na kwa umuhimu huo huo ilikuwa ni ahadi ya kujengwa kwa kiwango cha lami, ambayo ilitolewa na Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete na pia ilikuwa ni ahadi ya Rais wetu wa sasa Mheshimiwa Dkt. John Magufuli kuwa hizi barabara zijengwe kwa lami. Kwa umuhimu huo huo katika Ziara ya Waziri pamoja na Naibu Waziri nao kwa wakati tofauti walitembelea hizi barabara na kuona umuhimu wake na sasa labda ningependa kama ilivyo kwenye swali langu la msingi, ni lini barabara ya Mbalizi – Shigamba – Isongole itajengwa kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa umuhimu huo huo ni lini barabara ya Itewe - Mlima Nyoka - Songwe ambayo ni by pass itajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Njeza kwa kufuatilia maendeleo ya Jimbo lake hususan mambo ya miundombinu. Maana yake hii naiona ni style ya Mpwapwa hii ni Lubeleje style, maana kila ukikutana nae anazungumzia juu ya barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme tu kwamba barabara hii natambua kwamba ni ahadi ya Viongozi, lakini nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Mbeya Vijijini kwamba barabara hii ya Mbalizi – Shigamba – Isongole iko kwenye mpango mkakati wa Wizara kwa ajili ya kuiboresha. Kwa hiyo pindi tukipata bajeti tutafanya usanifu wa barabara hii na kuanza kuijenga katika kiwango cha lami. Vilevile kuhusu barabara hii ya Uyole – Mlima Nyoka hadi Songwe ambayo ni by pass Mheshimiwa Mbunge anatambua kwamba usanifu ulifanyika na kupitia Jiji la Mbeya na anafahamu kwamba eneo hili ni la uzalishaji mkubwa, kuna pareto inazalishwa kwa wingi lakini kuna viazi vinazalishwa kwa wingi, kuna mazao ya mbao, hii ni barabara muhimu pia kuna mahindi yanazalishwa kwa mwaka mzima katika eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi leo mtaalam mwelekezi anakwenda kufanya mapitio ya barabara hii kwa sababu uko uelekeo sasa wa kupata fedha ya kuijenga barabara hii by pass muhimu ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge nitaendelea kuku- update, kukupa taarifa zaidi tuone namna tunavyokwenda, lakini niseme tu kwa wananchi wa Mbeya Vijijini kwamba tumejipanga vizuri sasa kuanza kuijenga hii by pass kwa ajili ya huduma muhimu katika eneo hili.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwa Bagamoyo, Mji Mdogo wa Mbalizi ulianza mchakato wa kuomba iwe ni Halmashauri ya Mji kwa muda mrefu sana. Je, ni lini Serikali itaipa Mbalizi kuwa na hadhi ya Halmashauri ya Mji? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wanavyofahamu Wabunge wengi sana humu, kuna mapendekezo mbalimbali ya maeneo mbalimbali kuanzisha mamlaka mpya lakini najua kwamba Mbalizi ni miongoni mwa maeneo ambayo yalikuwa katika mchakato wa kupandishwa hadhi, lakini nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba tuvute subira kwa sababu mpango wa Serikali wa sasa hivi wa maelekezo ni kutoanzisha mamlaka mpya lakini kwa vile jambo hili liko katika subira tuvute subira pale hali itakapokuwa sasa imekaa vizuri Mji wa Mbalizi ni miongoni mwa miji ambayo itapewa kipaumbele cha kwanza katika upandishaji wa hadhi. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kutokana na majibu hayo, inaonyesha kuwa mgodi huu utakuwa ni neema sana kwa nchi yetu kwa sababu ya uzalishaji wa hayo madini ya Ferro-Niobium ambayo ni muhimu sana kwa ujenzi wa madaraja, Reli ya Standard Gauge pamoja na mabomba ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa umuhimu huo, napenda kuuliza maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, je, ni kwa kiasi gani hayo madini ya Ferro-Niobium pamoja na Niobium yenyewe yataongezewa madini ya chuma? Ni kwa kiasi gani haya madini ya chuma tutatumia madini yanayochimbwa hapahapa nchini kwetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vilevile imeonyeshwa kuwa kuna fidia kwa ajili ya Gereza la Songwe. Je, mwekezaji au wawekezaji wana mkakati gani badala ya kutoa fidia tu lakini waboreshe miundombinu ya gereza hilo ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya barabara, vituo vya afya na huduma zingine za elimu hasa kwa wananchi wa Kata ya Bonde la Songwe ambapo kiwanda hicho na mgodi huo upo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Ferro- Niobium ni matokeo ya uchakataji wa madini hayo utakaofanyika. Pale Mbeya uchimbaji utakuwa ni wa Niobium peke yake lakini Niobium haiwezi kutumika peke yake ni mpaka pale utakapoichanganya na iron, ndiyo maana tunaita Ferro-Niobium kwa maana ya kutengeneza high strength low-alloy, kwa maana ya material ya kuunganisha vyuma. Ndiyo maana Mheshimiwa Mbunge anasema kwamba itatumika kwenye madaraja na kwenye pipes, ni kweli madini haya yakishakuwa Ferro-Niobium yanatumika katika kuunganisha vyuma vikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge analitambua hilo na sisi kama Serikali tunalitambua hili. Kwa umuhimu wa material haya ndiyo maana katika jibu la msingi nimesema kwamba hii kampuni ikishaweka pale kiwanda, kwa maana ikishachimba Niobium itachanganywa na hiyo Ferro kwa maana ya iron kisha itauzwa nchi za nje. Kwa mfano, Amerika Kaskazini wanahitaji sana bidhaa hii kwa ajili ya utengenezaji au uunganishaji wa vyuma vikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni material ambayo yanahitajika sana duniani na sisi kama Serikali tunatambua. Tunasema kabisa kwamba tukishaweka kiwanda hiki pale, wakishachimba Niobium yetu haitatosha mahitaji kwa sababu itakuwa ni kiwanda peke yake Afrika ambacho kitakuwa kimejengwa pale Songwe na Niobium itakayohitajika, itahitajika hata ile ambayo ni nje ya Tanzania, ina maana Congo na Zambia wataleta Niobium yao hapa. Kwa hiyo, tutatumia Niobium karibu ya Afrika nzima katika kiwanda hiki ambacho kitajengwa Songwe. Kwa hiyo, tunatambua umuhimu wa kiwanda hiki na sisi kama Serikali tumeshikamana kihakikisha kwamba sasa tunakwenda kuhakikisha machimbo haya yanaanza na utengenezaji wa kiwanda kwa maana ya kuongeza thamani kinaanzishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, tunatambua kweli machimbo au mgodi huu, yako chini ya Gereza la Songwe. Tunapenda kusema kwamba ile ziara ya Mheshimiwa Rais aliyokuwa amekwanda Mbeya imekuwa ni chachu kubwa sana kuhakikisha kwamba zile mamlaka husika kwa maana ya Wizara ya Mambo ya Ndani, Uwekezaji tunakweda kukaa pamoja kuangalia ni namna gani sasa mwekezaji huyu atalipa fidia na kuweza kuhamisha gereza lile kulipeleka pembeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua yuko tayari kulipa kiasi cha dola milioni saba kujenga gereza jipya ambalo litabeba wafungwa 500 na kujenga nyumba mpya kwa ajili ya wafanyakazi zaidi ya 120 na ataweka miundombinu ya umwagiliaji pamoja na barabara kuhakikisha kwamba anaboresha maisha na mazingira ya gereza lile ambalo litajengwa pale pembeni. Kwa hiyo, mamlaka husika zinafanya kazi kuhakikisha kwamba tunamsaidia mwekezaji huyu na masuala yote ya kodi tumeshayaweka sawa, tuna hakika kabisa tutakwenda kuanza mradi huu muhimu kwa Tanzania. Ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Na mimi napenda kujua pamoja na ujenzi wa hii reli ya Mtwara –Mbambabay, Serikali ina mkakati gani wa kujenga reli kati ya Inyala (Mbeya) na Kyela kwenye Ziwa Nyasa ambayo itakuwa ni kiungo kizuri kuunganisha reli ya TAZARA pamoja na Bandari yetu ya Mtwara?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, reli ya TAZARA ilijengwa kwenye miaka ya 1975. Sasa hivi Serikali ya Tanzania na Zambia tunafanya ukarabati mkubwa pamoja na kuongeza vichwa na mabehewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Ziwa Nyasa tumejenga matishari matatu ambayo tayari yanabeba mzigo. Hata hivyo, baada ya kukamilisha ukarabati huu na kuimarisha ili reli ile iweze kubeba mzigo uliotarajiwa wa tani milioni 5 kwa mwaka, basi tutaanza na stadi kwa ajili ya kuunganisha hicho kipande cha kutoka Mbeya kuelekea kule Kyela.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupewa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nipende tu kuwashukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, waliweza kufanya ziara katika Jimbo la Mbeya Vijijini na katika ziara hiyo waliahidi kuwa wangepeleka umeme katika Kata za Maendeleo, Itawa na Shizuvi, ikiwa ni pamoja na vijiji vinavyolizunguka Jiji la Mbeya. Sasa je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye Kata za Maendeleo, Itawa na Shizuvi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tulitembelea Mkoa wa Mbeya, hususan Jiji la Mbeya na si chini ya mara mbili na kuwaahidi wananchi wa Kata za Maendeleo na Kata ambayo ameitaja ya Itawa, kwamba tutawapatia umeme na hususan katika mradi unaoendelea wa ujazilizi awamu ya pili, mzunguko wa kwanza, ambao hatua za manunuzi zimeshakamilika na kiasi cha shilingi bilioni 169 zimetengwa. Mkoa wa Mbeya ni miongoni mwa mikoa tisa ambayo itapata fursa ya ujazilizi awamu ya pili, mzunguko wa kwanza kama ambavyo imepata fursa ya ujazilizi awamu ya kwanza kutokana na mahitaji makubwa. Kwa hiyo nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na nimuahidi kwamba maeneo haya yatapatiwa umeme katika mradi ambao utaanza Julai, 2019. Ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwanza nianze kuipongeza Serikali na kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya maji katika Wilaya ya Mbeya.

Mheshimiwa Spika, pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa bajeti ya ziada ya shilingi bilioni 3.3 kwa ajili ya mradi wa maji uliotolewa kwa ajili ya Mji wa Mbalizi pamoja na Kata za Bonde la Songwe na Ilota. Pamoja na pongezi hizo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ni lini miradi ya maji itapelekwa kwenye Vijiji vya Ilembo, Santilia, Inyala pamoja na Ikukwa ambapo kunajengwa vituo vya kisasa vya afya na pia kuna Hospitali ya Wilaya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini sasa Mradi wa Mbalizi utakamilika kuhakikisha wananchi wa Bonde la Songwe, Ilota na Mji Mdogo wa Mbalizi wanapata huduma ya maji ya uhakika? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayofanya katika Jimbo lake. Sisi kama viongozi wa Wizara, mimi pamoja na Waziri wangu tulishafika kule kuhakikisha Mradi wa Mbalizi wa kiasi cha shilingi bilioni 3 tunausimamia ili ukamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sasa hivi baadhi ya kazi zinafanywa na wataalam wetu wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mbeya. Ndani ya mwezi Machi, mradi ule utakamilika na wananchi wa Mbalizi watapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi katika Vijiji vya Santilia pamoja na Ilembo na Ikukwa tulipata fedha zaidi ya shilingi bilioni 25 za Lipa kwa Matokeo na wafadhili wa DFID na Kijiji hiki cha Santilia kipo. Sasa tupo katika hatua ya manunuzi kuhakikisha tunaukarabati mradi ule na wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji.

Mheshimiwa Spika, nachotaka kumhakikishia kwa Vijiji vya Ilembo na Ikupwa katika awamu hii inayokuja ya fedha za Lipa kwa Matokeo tutaviweka katika kuhakikisha nao wanapata huduma hii muhimu sana ya maji. Ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, na inavyoonesha Benki ya Kilimo bado ina mahitaji ya mtaji mkubwa hasa ukizingatia kuwa kilimo kwa nchi yetu ndiyo tunakitegemea kwa kiasi kikubwa kwenye uchumi. Sasa ukiangalia katika jibu kwa Mkoa wa Mbeya ambayo imeoneshwa kuwa zimepelekwa shilingi milioni 700 lakini na hizi Wilaya alizozitaja Mheshimiwa Waziri siyo za Mkoa wa Mbeya ni za Mkoa wa Songwe. Kwa hiyo kwa jibu hilo inaelekea kabisa Mkoa wa Mbeya haujanufaika na mikopo ya Benki ya Kilimo.

Sasa swali langu; je, ni kwa kiasi gani Serikali imeweza kufanya tathmini ya mahitaji halisi ya mtaji wa Benki ya Kilimo? Na je, mtaji huo utapelekwa Benki ya Kilimo ukiondolea mbali hiyo mikopo ya ADB utapelekwa lini huo mtaji kwa Benki ya Kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kiasi kikubwa ukiwapa wakulima mikopo risk kubwa iko kwenye bei kwa sababu bei za mazao hazieleweki, kuna risk sana kwenye bei. Sasa kwa kiasi gani Benki ya Kilimo kwa kutumia instruments za kibenki na vilevile kwa kusaidiana na taasisi zingine kama commodity exchange (TMX) zimeweza kutengeneza utaratibu wa kuondoa hiyo risk, wa ku-manage hiyo risk ambayo inatokana na changamoto za bei za mazao yetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza lenye (a) na (b), tathmini ya mtaji na utapelekwa lini; tathmini ya mtaji ilishafanyika na kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi tunaangalia njia nyingine za ku-finance benki yetu ya kilimo ili iweze kuwa na uwezo wa kuwakopesha wateja wake ambao ni wakulima wadogo, wa kati pamoja na wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu Bunge lako tukufu likafahamu kwamba mabenki yote hayakopeshi kupitia mtaji, yanakopesha kupitia njia nyingine, co-financing agreement, ndiyo maana Serikali ilitafuta mkopo wa bei nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika na ikaipatia Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania. Kwa hiyo, hilo naomba Waheshimiwa Wabunge tulifahamu; hakuna benki yoyote inayokopesha kupitia mtaji wake, inakopesha kupitia amana na njia nyingine za utafutaji wa fedha ili iweze kuwahudumia wateja wake. Serikali ipo tayari kabisa kuiwezesha benki yetu kupitia mipango mingine ili ipate fedha za kutosha za kuwahudumia wakulima wetu ambao ndio lengo kubwa la uanzishwaji wa benki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la risk ya masoko; TMX ambalo ni Soko la Bidhaa Tanzania, limeanza kazi vizuri mwaka huu na tayari tumeona baadhi ya mazao kwa mfano ufuta ambao umetafutiwa soko zuri na Soko letu la Bidhaa Tanzania wameweza kutafuta masoko na sasa tunaendelea kutafuta masoko mengine kupitia Soko la Bidhaa Tanzania kwa ajili ya mazao yaliyobaki ili kuwasaidia wakulima wetu kuondokana na vihatarishi vya ukosefu wa bei au bei isiyoeleweka kwenye masoko yetu.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Napenda tu kuuliza Serikali, tuna mradi mkubwa wa uchimbaji wa madini ya niobium katika milima ya Panda Hill Songwe; na kwa bahati nzuri ile miradi ita-attract direct investment ya karibu dola milioni 200 na wawekezaji wapo tayari; na katika ziara ya Mheshimiwa Rais alipofanya ziara kule Mbeya…

MWENYEKITI: Swali, swali!

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu: Je, ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa kuwaruhusu hao wawekezaji waanze kuchimba haya madini ya niobium ili vile vile wajenge na kiwanda cha kuchakata hayo madini ambacho ni cha kwanza Afrika na cha nne duniani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kusema kwamba tunatambua kuhusiana na mradi huu wa Niobium ambao utafanyika katika milima ya Panda Hill na bahati nzuri nami nilipata bahati ya kukaa katika Wizara ya Madini, niliweza kuwaona wawekezaji hawa; na ni madini ambayo kwa kweli ni ya muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tulishaanza kuwashughulikia, pia tumekuwa na mashauriano na Wizara ya Madini pamoja na Wizara ya Viwanda kupitia EPZ. Tutakutana pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Madini pamoja na Wizara ya Viwanda ili kuweza kuona ni kwa namna gani tunakwamua mradi huu muhimu.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana ningependa kuuliza swali la nyongeza mji mdogo wa Mbalizi ulipewa mamlaka miaka 15 iliyopita na sasa hivi ina wakazi zaidi ya 100,000 na pia uwanja wa kimataifa wa Songwe uko katika eneo hilo. Sasa ni lini Mji mdogo wa Mbalizi utapewa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi ni kwamba kwa sasa tunaendelea kuimarisha maeneo ya kiutawala yaliyoanzishwa. Wanapozungumzia kuanzisha halmashauri maana yake unaongezea miundombinu unahitaji huduma ya ukubwa zaidi na watendaji watakuwepo na majengo yataongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuvumilia tuimarishe kwanza hii miji midog iliyopo halmashauri zetu na katika nchi hii kuna mikoa mingi pia bado haina majengo ya kutosha ya kuwa mikoa na watendaji wengine. Tuna upungufu wa miundombinu katika halmashauri zetu pia Waheshimiwa Wabunge wenyewe bado wanadai ofisi za Wabunge hazijajengwa. Kwa hiyo, nadhani ukiangalia mahitaji yaliyopo na kuongeza eneo la utawala nadhani tupeane muda kidogo tutekeleze haya yaliyopo tukamilishe tutazingatia baadaye maoni yake, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini kwa umuhimu wa kipekee wa biashara ya bandari yetu na nchi jirani naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni bandari shindani na bandari yetu ya Dar es Salaam zimekuwa zikiongeza jitihada za kuhakikisha kuwa wanafikisha huduma kwenye maeneo ambayo yalikuwa ni miliki ya bandari yetu ya Dar es Salaam hada DRC Katanga, Zambia na Malawi. Kutokana na ushindani huo biashara yetu ya shehena kwenda maeneo hayo kwa Zambia imepungua mpaka asilimia 25 sasa hivi, na vilevile kwa DRC Katanga nako ni chini ya silimia 25; ni asilimia 21 kutoka asilimia 40. Sasa swali langu nauliza, pamoja nakuboresha na ujenzi wa Bandari Kavu ya Inyala;

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga sasa barabara ya kutoka Mbalizi – Shigamba – Isongole ambayo inapitia katika eneo la Bonde la Songwe na kwenda mpakani na Malawi?

Ni lini itajenga reli ya TAZARA kutoka Tunduma kwenda Bandari za Ziwa Tanganyika kwa ajili ya biashara yetu na DRC Katanga? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Oran Njeza kwa jinsi ambavyo anafuatilia masuala ya kimkakati ya eneo lake. Ni kweli kwamba wananchi wa Mbeya Vijijini wamepata Mbunge jembe ambaye sidhani kama atakuwa na mpinzani.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ametaka kujua mpango wa Serikali wa kuimarisha barabara ya kutoka Mbalizi – Shigamba kwenda Isongelo ambayo itaunganisha na Wilaya ya Ilenye ukoje. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari kwa mwaka ujao wa fedha tumeshatenga fedha kwa ajili ya kufanya upembezi yakinifu, kisha tutafanya na usanifu wa kina kwa ajili ya kuiimarisha barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Kwa sababu tunajua kwamba kujenga Bandari ya Inyala bila ya kuwa na barabara ambayo ni imara itakuwa haiwezi kusaidia, kwa hiyo tunamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaijenga kipande hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye swali lake la pili anataka kujua kipande cha reli kitakachojengwa kutoka Tunduma hadi Bandari ya Kasanga Ziwa Tanganyika. Ni kweli kupitia Mamlaka ya Bandari Tanzania wanashirikiana na TAZARA kuhakikisha wanaweka miundombinu itakayokuwa wezeshi na rahisi kidogo kufikia Bandari ya Kasanga, Hivyo, kwa sasa wameshaanza upembuzi yakinifu wa kuhakikisha kwamba kipande cha reli kinatandikwa na watakapomaliza upembuzi yakinifu watafanya usanifu wa kina kupata gharama kwa ajili ya kupanga bajeti sasa ya kutekeleza mradi huo. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo kwa majibu yake mazuri na mkakati uliopo, lakini ukiangalia mkakati wa kuongeza uzalishaji kutoka tani elfu mbili, elfu tatu, elfu mbili mia nne kufika elfu tatu na mbia mbili hiyo bado ni asilimia 25 tu ya mahitaji ya dunia. Sasa kwa vile pareto inatumika kwa ajili ya kuua wadudu na hasa dawa za kuhifadhi mazao ambayo itapunguza cost, post harvest loss kwa nafaka zetu. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri agizo lake alilolitoa kuhusu taasisi yetu ya TARI ili waweze kuanza kufanya utafiti wa kuzalisha dawa kwa ajili ya kuondoa hii post harvest loss, lakini vilevile na dawa kwa ajili ya kuuwa wadudu wa mbu, ni lini hilo agizo lake litaanza kutekelezwa? Nafikiri ni muhimu sana tukichukulia ushindani ulioko kwenye nchi zetu za Afrika Mashariki wenzetu Kenya pamoja na Rwanda kama ulivyosema wewe mwenyewe wameshaanza huo uzalishaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa vile Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumzia kuhusu zoning ambayo hairuhusu wanunuzi wengi kwenye eneo moja. Hiyo limekuwa ni changamoto kwa bei ya pareto kuwa ndogo sana kwa vile kunakuwa na monopoly ya hao wanunuzi. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuna umuhimu wa kuruhusu wanunuzi wengi kwa kila eneo ili kuwepo na bei ya ushindani? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyingeza ya Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza agizo ambalo tumelitoa mwaka jana Serikali na sekta ya kilimo inatumia zaidi ya bilioni 150 kwa mwaka kwa ajili ya kununua input kwa maana ya gharama za viuatilifu na vitu vya namna hiyo. Ni kweli kwamba, pareto ni moja ya zao ambalo linaweza kutupunguzia gharama kwa kiwango kikubwa cha uagizaji wa viuatilifu. Wizara ya Kilimo mwaka jana tumewapa agizo watu wa TARI, hivi sasa tunavyoongea utafiti unaendelea ukihusisha sekta binafsi pamoja na kampuni ya PCT ambayo ndio kiwanda pekee kinacho-process kwenda kwenye crude level uzalishaji wa maua haya kwa ajili ya kupatikana dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuwahamasisha sekta binafsi ya Tanzania, ni commitment ya Serikali kuanzia taasisi zetu kama NFRA na CPB kuanza kutumia unga unaotokana na pareto kuzuwia wadudu waharibifu wanaoingia katika mazao kama mahindi na hii itatuongezea soko la ndani. Sisi kama Wizara tunatoa commitment kama kuna muwekezaji yeyote ambaye atazalisha kiuatilifu kinachotokana na pareto kwa ajili ya matumizi ya viuatilifu ndani ya nchi yetu tutampa contract ya kuhudumia zao na taasisi ambazo ziko chini ya Wizara ya kilimo. This is a commitment na tuko tayari kwa hiyo, tunahamisha sekta binafsi kuwekeza. Namfahamu Mheshimiwa Njeza ni mdau katika sekta hii na Mheshimiwa Rais alisema mabilionea karibu Wizara ya Kilimo tujadiliane juu ya hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu zoning. Hatuwezi kuondoa zoning kwenye suala la uwekezaji. Ni unfair mwekezaji kampatia huduma mkulima, kampa mbegu, kampa dawa, kampa ugani, halafu umruhusu mtu ambaye hajawekeza aende akanunue zao ambalo mwenzake kawekeza. Tutaendelea ku-protect zoning katika eneo hili, lakini tutafungua milango kwa yeyote anayetaka kuja kuwekeza kwenye sekta ya pareto, ili tuweze kuwapa thamani wakulima wetu na sisi ndani ya Wizara ya kilimo we are open for this. Nashukuru.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nashukuru vile vile kwa majibu ya Serikali ambayo yanaleta matumaini sasa kwa matumizi ya chuma na matumizi ya niobium na kuwepo kwa kiwanda cha FerroNiobium hapa hapa kwetu nchini. Swali la kwanza, je, sasa kwa vile haya madini inaonesha kuwa ni madini ya viwandani ambayo yatachanganywa pamoja na chuma na ikiwezekena pamoja na aluminium, ni lini sasa Serikali itahakikisha kuwa uzalishaji wa chuma ikiwemo machimbo ya Liganga na Mchuchuma yataanza mara moja ili yaweze kutengenezwa FerroNiobium hapa hapa nchini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa sababu haya madini yanatengeneza FerroNiobium, je, viwanda vya FerroNiobium vinaangukia kwenye Sheria za Uwekezaji za EPZ? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba madini ya Niobium yatachanganywa pamoja na madini ya chuma ili kutengeneza muunganiko huu wa FerroNiobium na ni kweli kwamba Serikali kwa sasa iko katika mazungumzo rasmi na mwekezaji anayewekeza katika Mradi wa Liganga ili hatimaye tuweze kuanza mradi huo kwa sababu umechelewa sana. Kwa hiyo napenda kuamini kwamba maongezi haya yatakapokuwa yamekamilika baina ya mwekezaji wa Liganga na suala likiwa hasa katika mikataba, basi mtanzuko huo utakapokuwa umeondoka tunapenda kuamini kwamba itakuwa ni fursa ya kuendeleza mradi wa Niobium ambayo itachanganywa na chuma chetu cha Liganga.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, ni kweli kwamba madini mengine yana matumizi katika viwanda na pia ndiyo iliyokuwa ni sticking point katika mazungumzo yetu na mwekezaji. Sasa ukiangalia madini ya Niobium katika periodic table ni transition metals, kwa hiyo tunapaswa tuyatambue kwamba ni madini ya metali na ukiyabadilisha yakaonekana kwamba kwa vile yana matumizi katika viwanda tozo inayotozwa ya royalty madini ya viwanda ni asilimia tatu, madini ya metali ni asilimia sita.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hapa napo tulikuwa na mkinzano na mwekezaji kwamba matumizi ya baadaye yasitusababishe tukaanza kuonesha kwamba hayako katika group la metali, kwa sababu hata dhahabu nayo pamoja na kwamba ni metali inaweza ikapata matumizi katika viwanda. Kwa hiyo tukaona kwamba hebu tuendelee kuuangalia upande wa kwamba madini ya niobium ni madini ya metali, royalty yake ibakie kuwa asilimia sita hata kama baada ya hapo itakuja kuchanganywa na kuwa FerroNiobium. Kwa hiyo hayo ni maongezi ambayo tumeongea na mwekezaji na tunaamini kwamba tutafikia muafaka. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza na nishukuru kwa jibu kutoka kwa Wizara ya Elimu. Kutokana na umuhimu wa huduma ya afya na hasa kwa suala zima la kupatikana kwa wahudumu pamoja na madaktari katika kipindi hiki ambacho milipuko ya magonjwa imepamba moto. Je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia ardhi ya Taasisi za Serikali zilizopo katika Wilaya ya Mbeya ikiwemo ardhi ya Tanganyika Packers ili iweze kukidhi mahitaji ya chuo hiki?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, hii Ndaki ya Afya ina mkakati au mpango gani wa ziada zaidi ya kufundishia ili tuweze kupata huduma nyingi kutokana na hili eneo kubwa ambalo watakuwa wamepatiwa sasa hivi na Serikali? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli anayozungumza Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna mkakati wa kupata eneo hilo amelizungumza linalomilikiwa na Tanganyika Packers, ambalo liko chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Wizara yangu ikishirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi lakini vilevile Wizara ya Ardhi pamoja na Menejimenti ya Chuo na Uongozi wa Wilaya tutahakikisha tunakwenda kupata umiliki wa eneo hilo ili kuweza kufanya ujenzi wa chuo hiki.

Mheshimiwa Spika, pindi tutakapopata eneo hili, basi Serikali inaweza kutenga bajeti sasa kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga hospitali kubwa ambayo pamoja na Ndaki hii inaweza kuambatanishwa na Ndaki nyingine ili kuweza kupata wataalam wengi zaidi kwa ajili ya kuhudumia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo, mkakati wa muda mrefu kama nilivyozungumza mwanzo ni kwamba Serikali inatambua jambo hilo na tutakwenda kushughulikia kwa kadri bajeti itakavyoruhusu. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Marais wetu waliopita akiwemo Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli waliahidi ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi – Shigamba:-

Je, ni lini sasa hiyo barabara itajengwa kwa kiwango cha lami? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ahadi zote za Viongozi Wakuu wa Nchi akiwemo Dkt. Hayati Magufuli, Mama Samia, Mheshimiwa Waziri Mkuu na viongozi wengine, ahadi hizi lazima zitekelezwe kwa sababu ni ahadi ya Serikali na Serikali ipo kazini inafanya kazi na kazi inaendelea.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwaa Mbunge kwamba, barabara yake hii kama ilivyoahidiwa itafanyiwa kazi, itajengwa kwa kiwango cha lami, tupeani ushirikiano na muda si mrefu ahadi hiyo ya viongozi itatimia kabla ya 2025. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pia nashukuru sana kwa Mheshimiwa Naibu Waziri na hata pacha wake kwenye Wizara hiyo, wanaifahamu sana jiografia ya Wilaya ya Mbeya na hasa Mbalizi. Swali la kwanza, ahadi nyingi zimetolewa, hata wewe utakumbuka kuwa, eneo la miteremko ya Iwambi – Mbalizi lina ajali nyingi na zinaendelea. Mheshimiwa Rais wa sasa tarehe 15 alipotembelea na kuwapa pole wananchi wa Mbalizi kwa ajali mbaya iliyoua watu zaidi ya 20, aliahidi ujenzi wa Barabara ya By-pass ya Uyole – Songwe na By-pass ya Mbalizi – Iwambi. Sasa ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; bandari kwa muda mrefu walitwaa eneo la Inyala kwa ajili ya ujenzi wa Bandari Kavu, lakini kwa miaka mingi sasa hawajaweza kuwalipa wananchi na wananchi hawafanyi shughuli zozote za uzalishaji. Sasa ni lini Wizara itaipa nafasi na kuiamuru Mamlaka ya Bandari walipe fidia kwa wananchi wa Inyala, Mbeya? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni kweli kwamba, Mheshimiwa Rais, Mama Samia, alipita katika eneo ambalo ametaja na akatoa maelekezo. Bahati nzuri tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kupitisha bajeti yetu jana na miongoni mwa fedha ambazo zimetengwa ni pamoja na malipo ya Barabara hii ya By-pass pale Uyole – Songwe. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge awe na amani tutakapoanza utekelezaji wa bajeti hii hili eneo tutazingatia maelekezo ya kiongozi mkuu wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, anazungumza habari ya fidia ya Bandari Kavu, Inyala. Miongoni mwa maeneo muhimu ambayo tumepanga kujenga Bandari Kavu ni pamoja na Inyala, ambayo itahudumia ukanda wa Nyanda za Juu Kusini. Kwa hiyo, kwa sababu anasema kwamba, kuna shida pia ya mawasiliano naomba nimhakikishie kwamba, shida hiyo itamalizika fidia iweze kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukubaliane baada ya maswali na majibu tuongee na Mheshimiwa Mbunge tupate exactly hasa malalamiko yako wapi, ili utekelezaji wa jambo hili ufanyike, wananchi walipwe fidia zao, wafanye shughuli za maendeleo, lakini pia bandari hii ijengwe na Serikali iweze kumiliki eneo hili ili na kupunguza migogoro kati ya wananchi na Serikali yao pendwa ya Chama Cha Mapinduzi.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa swali la nyongeza; lakini vile vile, naomba niishukuru sana Serikali kwa kweli kwa kazi kubwa iliyofanya ya kusambaza umeme vijijini. Ninashukuru sana ya kwamba vijiji 39 vya mwisho sasa navyo kazi imeshaanza ili kukamilisha vijiji vyote vya Wilaya yetu ya Mbeya, Halmashauri ya Mbeya Jimbo la Mbeya Vijijini kupata umeme, nashukuru sana kwa hilo; ingawaje mkandarasi alipewa vijiji 32 kwa hiyo nitamuomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia ili kuoanisha hayo mahesabu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa mradi mkubwa wa Tanzania Zambia Inter-Conector ambao unapita kwenye vijiji vya kata nane za Wilaya ya Mbeya Jimbo la Mbeya Vijijini. Inapita katika Kata za Ulenje, Inyala Maendeleo, Itewe, Swaya, Igale, Iwindi na Bonde la Songwe. Wananchi waliopisha ujenzi wa line hii waliahidiwa kupatiwa fidia tangu mwaka 2018, lakini mpaka leo hii wanasubiria hakuna kinachoendelea, na imekuwa kero kwa vile waliambiwa wasifanye ujenzi wala maendeleo yoyote. Sasa ni lini wananchi hawa watapata fidia yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kama unavyojua kupeleka umeme vijijini ni kuchochea uchumi, lakini kumekuwa na mkanganyiko wa tozo kati ya wateja wa line ya three phase na wateja wa line ya single phase. Wateja wa line ya three phase wanatozwa na TANESCO Shilingi 918,000 ambapo REA wanawatoza 139,000.

Je, Serikali ina mpango wa kuoanisha hizo tozo mbili ili kuchochea huo uchumi vijijini na wananchi waweze kulipia laki moja na thelathini na tisa badala ya laki tisa na kumi na mbili? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Manase Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake na shukrani alizozitoa kwa Serikali, na mimi kwa niaba yake nizipokee, kwamba Serikali imejitahidi sana kuhakikisha inapeleka umeme vijijini na katika maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba vijiji 39 ambavyo anavyo vyote vitapata umeme pamoja na kwamba inawezekana mkandarasi alipewa 32 vya kwanza. Pia niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kwamba hata kama mkandarasi alipewa vijiji pungufu ya vile ambavyo uhalisia vimebaki, katika survey hii ambayo tumewatuma wakandarasi wafanye kwenye maeneo yetu watahakikisha na vile vijiji vingine ambavyo vilibaki au viliachwa vinachukuliwa katika kazi zao na katika adendum za nyongeza za kazi tutakazo wapatia, watavichukua vijiji vyote na kuvifanyia kazi. kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ufuatiliaji wake umefanikiwa na wengine pia umeme utapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la fidia itakayolipwa kwenye mradi mkubwa wa kuunganisha umeme wa grid kutoka Iringa kwenda Mbeya, Tunduma mpaka Sumbawanga, takribani kilomita kama 622, kazi hiyo ya umbembuzi yakinifu imefanyika imekamilika na sasa makabrasha ya ulipaji wa fidia ndiyo yanawasilishwa sasa kwenye ofisi zetu kwa ajili ya uhakiki na kuweza kulipa fidia hiyo. Kwa hiyo bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri aliwasilisha hapa juzi imetenga kiasi cha kuanzia, zaidi shilingi bilioni moja kwa ajili ya malipo ya fidia ya eneo hilo, na tutaanza kulipa fedha hiyo kuanzia kwenye mwezi wa kumi na kuendelea kwa ajili ya kupisha sasa ujenzi wa mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, niombe kutoa maelezo na maelekezo kwa watumishi wenzetu. Serikali imesikia kilio cha Watanzania na tayari ilielekeza kwamba umeme katika maeneo yote utaunganishwa kwa shilingi 27 kwa umeme mdogo. Kwenye maeneo yetu ya vijiji Serikali imetoa msamaha wa kuunganisha line ya nguvu kubwa three phase kwa gharama ya shilingi 139,000 tu. Kwa hiyo, ninawaelekeza watumishi wenzetu wa TANESCO kwamba maeneo yote ya vijijini ambapo either ni TANESCO kapeleka umeme au REA imepeleka umeme, gharama ya kuunganisha umeme wa three phase ni shilingi 139,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo shilingi 912,000/= ni kwenye maeneo mengine ya mijini ambapo mradi wa REA wowote ule haujafika. Kwa hiyo ieleweke wazi kabisa, waheshimiwa Wabunge tunaomba tusaidiane katika usimamizi wa hili. TANESCO akiwa analeta umeme au REA analeta umeme mkubwa gharama yake ni shilingi 132,000 kwenye maeneo yetu ya vijijini. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hali ya madaraja ya TAZARA, hasa kwa upande wa mataruma ya mbao, yana hali mbaya sana kiasi cha kuhatarisha maisha ya wasafiri pamoja na usalama wa mizigo. Je, Serikali ina mkakati gani na mpango wa haraka kupeleka fedha ili hayo madaraja yaweze kukarabatiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; TAZARA ni muhimu sana katika ushindani wa Bandari yetu ya Dar es Salaam, huu ushindani wa kikanda unaifanya bandari yetu kuwa katika pressure kubwa sana. Je, Serikali haioni umuhimu wa kutenga pesa ya kutosha kupitia TPA Shirika letu la Bandari ili liweze kushiriki katika kujenga na kuboresha miundombinu ya TAZARA? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, anatoa taarifa ya hali mbaya ya Reli yetu ya TAZARA. Ninaomba nimuelekeze Mtendaji wetu wa TAZARA atembelee maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja, afanye tathmini ya haraka ili tuone kama hali ni mbaya kiasi hicho Mheshimiwa alivyozungumza basi ufanyike utaratibu wa kawaida kufanya marekebisho ili kuepuka madhara kwa mizigo na abiria ambao wanatumia eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge anauliza kama kuna uwezekano wa TPA kuwekeza katika eneo hili. Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Kamati tumekutana kule TPA Dar es Salaam, wazo hili alilitoa ni wazo jema. Tumewapa maelekezo watu wa TPA waangalie uwezekano wa kuwekeza katika eneo hili kwa sababu wanaihitaji TAZARA katika kusafirisha mizigo, walifanyie kazi, wafanye tathmini, tukijiridhisha basi wazo la Mheshimiwa Mbunge tutalifanyia kazi. Lengo ni kuweza kutoa huduma kwa watu wetu, hasa upande wa Tanzania. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa ni ahadi ya muda mrefu ya viongozi kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya Mbalizi - Shigamba. Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara imeahidiwa na viongozi mbalimbali wametoa ahadi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara hii ipo kwenye mipango ya kuanza kufanyiwa usanifu wa kina kama maandalizi ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Inaelekea kuna mkanganyiko kidogo kwenye majibu ya Serikali, kwa sababu mwaka 2007 wananchi wa Kata ya Ilungu hususan Kijiji cha Kikondo walifanyiwa tathmini ya kupewa fidia kwa yale maeneo yaliyochukuliwa na DAFCO ambayo sasa hivi ndiyo Hifadhi ya Taifa ya Kitulo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo wenzetu wa TANAPA walishindwa kuwafidia wale wananchi, kwa hiyo yale maeneo hasa Kijiji cha Kikondo bado yanatumika ni kijiji ambacho kina shule kina zahanati. Pia kuna maeneo ambayo yalichukuliwa na watu wa TFS kwenye Misitu ya Mwambalis na hayo maeneo yamekuwa yakitumiwa na wananchi hata kabla ya hapo na mpaka leo yanatumiwa.

Sasa kutokana na mkanganyiko wa majibu, naomba Mheshimiwa Waziri apange ziara akayatembelee hayo maeneo ili afanye tathmini yeye mwenyewe ili kujua uhalisia, lakini hali siyo nzuri kuna mgogoro na wananchi kwa kweli wanapata shida sana. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto hizi ambazo mara nyingi wananchi wamekuwa wakihitaji ardhi wakati huo huo maeneo haya yalichukuliwa na Serikali. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba changamoto hizi tutaenda kuzifuatilia, lakini pia tutaenda kukutana na wananchi ambao wamekutana na kadhia hii na lengo ni kukaa pamoja ili kuweza kutatua changamoto hii. Hivyo nitafika kwake kwenda kutatua changamoto hii. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. na mimi ninapenda kujua ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi – Shigamba ambayo ni kiungo cha mikoa ya Mbeya na Songwe kupitia Ileje, na pia ni kiungo kwenda Nchi jirani ya Zambia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbalizi – Shigamba tayari zabuni zinaandaliwa kuitangaza kwa ajili ya kufanya feasibility study na usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi kwa kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo mwaka huu tutahakikisha tunakamilisha feasibility study pamoja na usanifu wa kina, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza napenda nianze na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuanza utekelezaji wa kutoa ruzuku kwenye pembejeo za mbolea na zoezi hilo linaenda vizuri sana na wananchi wamepunguziwa mzigo mkubwa kwenye pembejeo za mbolea kupitia hiyo ruzuku pamoja na soko la dunia mbolea kupanda bei kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu; kwa sababu kimuundo Benki Kuu huwa inakopesha mabenki kwa muda mfupi na katika hali hiyo haiwezi kukidhi mahitaji ya mikopo ya kilimo ambayo ni ya muda mrefu. Sasa je, ni kwanini Serikali haioni kuhamisha huo mfuko kutoka Benki Kuu na kwenda Benki ya Maendeleo ya Kilimo, hizo shilingi trilioni moja ziweze kusaidia wakulima? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Njeza kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalichukua na kulifanyia tathmini, tukiona kwamba upo ubora wa kufanya hivyo, Serikali itachukua hatua stahiki. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nami napenda kujua ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha njia nne barabara kuu ya TANZAM, kipande cha Uyole mpaka Songwe kupitia Mbeya Jiji na Mbalizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Jiji la Mbeya ni kati ya majiji ambayo yana changamoto kubwa sana ya usafiri katika kipindi hiki; na Serikali ina njia mbili ya kutatua changamoto hizi. Moja, ni kujenga bypass ya kuanzia Uyole hadi Songwe yenye urefu wa kilomita 49; na pia kupanua barabara inayopita katikati kutoka njia mbili kwenda njia nne.

Mheshimiwa Spika, hatua ya haraka ambayo Serikali imechukua ni kupanua kwanza njia mbili kwenda njia nne kuanzia Uyole hadi Songwe eneo la Ifisi kilomita 29 na taratibu za manunuzi zinaendelea hadi tunavyoongea hapa sasa kwa mwaka huu wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORANI M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza kuipongeza Serikali kwa kuanzisha na vile vile kuboresha hii ndaki ya afya ikiwa sehemu ya uboreshaji wa Afya nchini kwetu. Sasa kwa vile kuna ongezeko kubwa sasa hivi la magonjwa yasiyoambukizwa: Je, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na hii ndaki ya afya wamejiandaa vipi kukabiliana na hilo ongezeko la magonjwa yasiyoambukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa hiki chuo kinaonekana kuwa kitakuwa na eneo kubwa sana, kwa hiyo, kinategemea kuwa na ongezeko kubwa la wanafunzi.

Je, kitakuwa na wanafunzi wangapi na pia wafanyakazi wangapi mara kitakapokamilika kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kawaida kwenye vyuo vyetu vikuu, jukumu lao la kwanza ni kuhakikisha kwamba utoaji wa taaluma ya aina mbalimbali au katika maeneo ambayo yanakuwa yameainishwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba chuo chetu cha tiba ya binadamu Muhimbili kinaendelea kufanya utafiti wa magonjwa haya yasiyoambukizwa kwa undani zaidi ili kujua chanzo cha magonjwa haya na namna gani tunaweza kuyaepuka. Kwa hiyo, nimwondooe wasiwasi, na mikakati yetu kama Serikali na kama Wizara ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kufanya tafiti hizo za kina.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni kuhakisha tunatoa elimu kwa Umma kuhusu namna gani ya kuepuka na kujikinga na magonjwa haya yasiyoambukiza. Kwa hiyo, hilo litakuwa ni jukumu la pili na mkakati wetu wa pili. Eneo la tatu ni kubadili sasa mifumo ya maisha yetu tuliyozoea kuishi ili kuweza kuepukana na magonjwa haya kama vile kubadili milo yetu na kuendelea kufanya mazoezi ya kila siku. Kwa hiyo, hiyo ndiyo mikakati yetu na tutahakikisha kwamba chuo kinaenda ku-emphasize kwenye mikakati ili kuhakikisha kwamba mambo haya yanakaa sawa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili linahusiana na suala la takwimu. Ameulizia wanafunzi watakuwa wangapi katika ndaki hii pamoja na watumishi watakuwa wangapi? Kwa vile sasa takwimu hizo sina hapa, naomba Mheshimiwa Mbunge aridhie kwamba tukimaliza Bunge hili tuweze kutafuta takwimu hizi na niweze kumpatia rasmi. Nakushukuru sana.
MHE. ORAN M. NJENZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa kuwa wananchi wa Kata ya Igoma, Wilaya ya Mbeya wameanza kujenga kituo cha kimkakati kwa kuhudumia kata jirani za Wilaya Rungwe, Wilaya ya Mbeya na Wilaya ya Makete ikiwemo Kitulo pamoja na TFC. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweza kuwaunga wananchi waliojenga mpaka Mtamba wa Panya ili wamalizie hicho kituo cha kimkakati angalau milioni 100 tu? Kama Serikali inaweza kuwapelekea hicho kituo kitafika hatua nzuri. Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunawapongeza wananchi wa Mbeya Vijijini pamoja na Mheshimiwa Mbunge wao kwa ushirikiano walioufanya na kuanza ujenzi wa Kituo cha Polisi Kata ya Igoma kama ilivyoelezwa na Mheshimiwa Mbunge. Ombi langu kwa uongozi wa Wilaya ya Mbeya wawasilishe maombi kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi ili kituo hiki kiingizwe kwenye mpango wa ujenzi kama ambavyo tumefanya kwenye maeneo mengine. Nashukuru.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa Barabara ya Mbalizi - Shigamba ni ahadi ya muda mrefu ya viongozi wetu na pia ni kiungo muhimu kwa Tanzania na Malawi. Je, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyoongea sasa hivi, Mhandisi Mshauri yuko site akifanya usanifu wa kina na baada ya hapo, barabara hii itatafutiwa fedha kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa katika Wilaya ya Mbeya, kuna madini ya aina ya calcium carbonate kwa wingi na NDC katika miaka ya 2006/2007 walikuwa na mkakati wa kuanzisha kiwanda ili watengeneze mbolea, CAN: Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kiwango hicho kwa kushirikiana na NDC?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa bei hizi za mbolea zinatishia upungufu mkubwa wa chakula: Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inarudisha ruzuku kama ilivyo kwenye nchi nyingine za SADC na Afrika Mashariki?

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza la ujenzi wa kiwanda, ni dhamira ya Serikali kuona ujenzi wa viwanda vingi zaidi vya mbolea vinakuwepo hapa nchini ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa mbolea na kupunguza bei ya mbolea na kupunguza bei ya mbolea kama ilivyo sasa. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Wizara pamoja na wenzetu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, tutakaa pamoja ili tuhakikishe kwamba wazo hili ambalo lilianzishwa mwaka 2006 liweze kukamilika na kuwapungizia adha wakulima.

Mheshimiwa Spika, la pili, ni la kuhusu ruzuku. Katika bajeti yetu ambayo tutaisoma mwezi ujao na pia katika utekelezaji ambao utaanza mwaka ujao wa fedha, tumedhamiria kutenga mfuko maalum (price stabilization fund) kwa ajili ya kudhibiti upandaji wa bei ya pembejeo ikiwemo na bei za mazao.

Mheshimiwa Spika, hivyo, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba hii ni sehemu ambayo pia tunaipa umuhimu mkubwa na Serikali imedhamiria kuanzisha mfuko wa ruzuku ambao utahakikisha unasaidia kupunguza maumivu ya wakulima na hasa katika upatikanaji wa bei ya mbolea ambayo itakuwa ni rafiki kwa mkulima.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Mimi ningependa kujua; kwa vile mchakato wa kupandisha hadhi ya Mji Mdogo wa Mbalizi, ambao ni mamlaka kuwa halmashauri ya mji ilishapitishwa kiwilaya na mchakato vilevile ulishapitishwa kimkoa. Je, ni lini sasa Serikali itaipandisha hadhi hii Mamlaka ya Mji kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante saa. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijiji kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge amesema katika swali lake taratibu za awali za Mbalizi kupandishwa hadhi kuwa Halmashauri ya Mji zilishafanyika, naomba tulichukue hilo tufuatilie kama lilishawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI, na baada ya hapo tutafanya tathmini kwa mujibu wa sheria na tutawapa mrejesho hatua ambayo itafuata. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa kuwa barabara ya Ishonje, Kikondo kuelekea Makete kwa muda mrefu sasa imekuweko kwenye bajeti ya kujengwa kwa kiwango cha lami.

Je, ni lini sasa hiyo barabara, hususan kipande cha Ishodye, Kikondo kuelekea Makete, itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekitti, Barabara aliyoitaja ya Ishonje Kikonde Makete ilitangazwa kilomita kama 25 haikupata mkandarasi. Lakini imetangazwa tena ambapo sasa tumeongeza hata kilometa siyo tena 25 ni kilomita kama 50, na ni mwendelezo wa barabara ya kutoka Njombe, Makete kuja Ishondye ambayo inaunganisha mkoa wa Mbeya na mkoa wa Njombe. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari barabara hii imeshatangazwa na ni taratibu tu za manunuzi ambapo tutaanza kuanzia Makete kuendeleza kwenda kuunganisha na mkoa wa Mbeya. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza na pia napenda nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa jibu lake zuri na pia kumpongeza Mheshimiwa Rais, kwa kutoa ruzuku kwenye pembejeo za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mikakati mizuri iliyowekwa na Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, hiyo mikakati hasa utoaji wa ruzuku utakuwa ni endelevu kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa sababu ruzuku ilikuwa kwenye mbolea lakini kuna pembejeo zingine kama mbegu hasa za nafaka, je, Serikali ina mkakati gani pia wa kutoa ruzuku kwenye pembejeo aina ya mbegu pamoja na viatilifu kwa ajili ya kilimo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa ruzuku ya mbolea unategemeana sana na bei ya mbolea duniani na namna ambavyo wakulima wetu wataweza kumudu gharama hizo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango huu ni endelevu kwa muda wa miaka mitatu na tutakuwa tunaendelea kuangalia bei za dunia na kama ikitokea kwamba wakulima wanazimudu gharama, mpango huu pia hautaendelea kwa sababu ni mpango wa kumsaidia kumlima kuondokana na machungu ambayo ameyapata kutokana na kupanda kwa bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu mbegu za nafaka. Moja kati ya mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kwamba, tunawafikia wakulima na kuwafanya wakulima wetu waweze kuzalisha kwa tija na eneo mojawapo ambalo tumekuwa tukiliangalia ni ruzuku kwenye eneo la mbegu na katika mwaka huu wa fedha tumefanya katika zao la ngano. Vilevile katika mahindi kupitia Wakala wa Mbegu Kilimo Tanzania, tumefanya hivyo kwa kushusha bei ambayo ni tofauti na bei iliyoko sokoni. Kwa mfano Mbegu za OPV za STUKA M1 zinapatika kwa Sh.2,750 tofauti na bei ilivyo sokoni, lakini mbegu za high breed za UH 6303 inauzwa kwa Sh.4,000 tofauti na bei iliyoko sokoni ya Sh.7,000, kwa hiyo ni sehemu pia ya ruzuku.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa wananchi waliopisha barabara ya Bypass ambayo ni mpya ya Uyole mpaka Songwe?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyotaja Mheshimiwa Njeza Mbunge wa Mbeya Vijijini, ni mpya, inajengwa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zinaendelea na barabara ambazo tunazijenga wananchi watafanyiwa tathmini na wakati tunaanza ama kabla hatujaanza, wananchi hawa watalipwa fidia zao, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa vile Mamlaka ya Mji mdogo wa Mbalizi kwa muda mrefu sasa imeshakua, na ina uchumi mkubwa, ni lini Serikali itaipandisha hadhi kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kuhusu kupandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo Mbalizi kuwa Halmashauri ya Mji, kwa sasa Serikali inamalizia kwanza majengo ya kiutawala na huduma za kijamii katika mamlaka ambazo zipo tayari. Baada ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu katika mamlaka hizi, tutaanza sasa kuangalia ni wapi panahitaji napo kupandishwa hadhi na kuwa mamlaka ya mji kama vile kule Mbalizi?
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri haya ya Serikali. Lakini naomba nikupongeze wewe mwenyewe kwa jitihada hizi na sasa kweli maendeleo ya Mbeya na Mbeya imetulia. Swali langu la kwanza je, ni lini sasa wananchi waliyopisha hii barabara wataanza kulipwa fidia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Kuna barabara ya kiungo muhimu cha Mkoa wa Songwe pamoja na nchi jirani ya Malawi. Barabara ya Mbalizi – Shigamba ni lini Barabara ya Mbalizi – Shigamba itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwamba barabara hii itaanza kujengwa kwa EPC+F ili kupunguza msongamano katika Jiji la Mbeya. Hii inaenda sambamba na ujenzi wa barabara ya njia nne kilomita 29 Uyole hadi Ifisi ambayo tayari Mkandarasi yuko site. Sasa kuhusu fidia ni kwamba fidia itaanza kulipwa mara tutakapokuwa tumehakiki wale wananchi wote ambao walishaainishwa kwamba watalipwa kwa mpango wa sasa kwamba kabla atujaanza kujenga hiyo barabara tutahakikisha kwamba fidia inalipwa kwenye barabara hiyo ambayo wananchi watapisha ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala lake la pili Barabara ya Mbalizi – Shigamba ambayo inakwenda mpaka Itumba – Isongole mpakani na Malawi. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba sasa hivi tunakamilisha na anafahamu Mheshimiwa Mbunge tunakamilisha kufanya usanifu wa kina na tunategemea mwaka huu tutakamilisha na baada ya hapo sasa utaratibu ni kuijenga barabara hiyo yote kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Napenda kuuliza barabara ya Bypass ya Uyole – Songwe, ni lini wananchi watalipwa fidia waliopisha hiyo barabara ya bypass?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE.ENG GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara inayotajwa ndiyo kwanza wakandarasi wameshakabidhiwa, na ipo kwenye huu mpamgo wa EPC+F. Jana nilijibu kwamba moja ya vitu ambavyo sasa hivi vinafanyika ni kupitia upya na kufanya tathmini ya malipo yatakayofanyika kwa ajili ya wale wananchi ambao watapisha, ikiwa ni pamoja na wananchi wa hiyo Barabara ya Uyole – Songwe Bypass. Ahsante.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naishukuru Serikali Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi alisharidhia kupandisha hadhi hiyo barabara kuwa ya Mkoa. Kwa vile hii barabara iko kwenye hali mbaya sana.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa hii barabara ili ianze kupitika?

Swali la pili, katika hali hiyo hiyo kuna barabara ya Ilembo - Isonso ambayo inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe. Je, ni lini hii barabara nayo itapandishwa hadhi kuwa ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza kwanza lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii ambayo tayari imeshapandishwa hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, barabara ikiwa imeshakidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na ikapandishwa hadhi na kuwa inahudumiwa na TANROADS basi ni wajibu wa TANROADS kutenga bajeti hiyo kuweza kutengeneza barabara. Tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na kuona wao wamejipanga vipi kwa ajili ya kutengeneza barabara hii ambayo ni muhimu sana kule Jimboni kwa Mheshimiwa Njeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara ya Ilembo-Isonso ambayo inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe lakini hasa katika Wilaya ya Ileje. Barabara hii itapandishwa hadhi pale ambapo watafuata vile vigezo vya kisheria kama ambavyo barabara nyingine zinafanya. Waanze vikao vyao katika DCC waende kwenye RCC na baadaye Bodi ya Barabara ya Mkoa na kisha kumwandikia Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi mwenye dhamana ya barabara hizi za Mkoa, ili timu iweze kutumwa kwenda kwenye barabara hii ya Ilembo - Isonso, kufanya tathmini na kisha kumshauri Waziri wa Ujenzi kuhusu barabara hii kupandishwa hadhi.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali na kwa hatua iliyofikiwa na hii itapelekea kukwamua hata makampuni makubwa na viwanda vikubwa ambavyo vilikwama kufunguliwa kutokana na kukosa umeme mkubwa. Pia kuna vijiji kadhaa na vitongoji kadhaa ambavyo vimekosa umeme kutokana na kuchelewa kwa mradi huu vikiwemo Vijiji vya Kata za Ulenje, Kinyara, Vijombe, Swaya, Igale, Iwindi na Bonde la Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; je, ni lini sasa Serikali itapeleka umeme kwenye Vijiji vya Ihango Kata ya Ulenje na Mina na Lusungo Kata ya Iwindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali ina mkakati gani wa kukwamua Mradi wa REA, awamu ya tatu, round ya pili, ambao umekwama kwenye Jimbo la Mbeya Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Oran Njeza kwa pamoja, kwa sababu yanahusu umeme vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Njeza pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote kwamba Mradi wetu wa Kupeleka Umeme Vijijini, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, utakamilika ifikapo Desemba. Vijiji aliyovitaja vilivyo katika kata hizo vyote vitakuwa vimepata umeme kufikia mwezi Desemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi anayepeleka umeme kwenye eneo la Mbeya Vijijini ni mkandarasi wetu ETDCO ambaye ni kampuni tanzu ya TANESCO na ameuliza ni jitihada gani zimefanyika kukwamua mradi kwenye eneo lake. Mkandarasi huyu sasa amewezeshwa zaidi na kampuni mama ya TANESCO, lakini na sisi kama Wizara tumeweka utaratibu mpya wa kusimamia miradi hii ikiwa ni pamoja na kuajiri vijana kwenye maeneo yetu ya majimbo, lakini kuajiri wakandarasi wahandisi wengi zaidi wa REA kwenye maeneo ya mikoa na kuweka ma - group ya kijamii ya WhatsApp, Waheshimiwa Wabunge wameyaona. Tunaamini kwa njia hizi na jitihada ikiwemo na kulipa pesa kwa wakati, miradi hii yote ya REA iliyokuwa inasuasua, itakamilika kwa wakati ikiwemo kwenye eneo la Mheshimiwa Njeza ambapo mradi utakamilika ifikapo Desemba kupitia makandarasi wetu wa ETDCO.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye vijiji vya Kata ya Shizuvi ambavyo ni sehemu ya REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, vijiji vyote ambavyo viko kwenye Mradi wa REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, vitakamilika ifikapo Desemba mwaka huu wa 2023. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Oran Manase Njeza kwamba vijiji hivyo pia katika kata hizo vitakuwa vimefikiwa na umeme kabla ya Desemba mwaka huu 2023.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naishukuru Serikali vilevile kwa vile Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi amesharidhia hii barabara sasa hivi kuhudumiwa na TANROADS, lakini iko kwenye hali mbaya sana. Sasa je, ni lini barabara hii itaanza ujenzi ili irekebishwe kuanzia Mjele, Ikukwa na siyo Ikuwa mpaka Mlima Njiwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika hali hiyo ya barabara, barabara ya Haporoto – Ileya – Ishinda ambayo inahudumia wachimbaji wa Migodi ya Ileya na Ishinda, ni lini barabara hii itapata matengenezo kwa vile nayo iko kwenye hali mbaya sana? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema, baada ya kupandishwa hadhi hiyo barabara, TANROADS itaanza utekelezaji kwa bajeti ambayo tunaanza kuitekeleza kwa 2023/2024. Kwa hiyo kwa sasa wenzetu wa TARURA baada ya Juni watatukabidhi na sisi tutaanza utekelezaji huo kwa bajeti mpya, ahsante. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa kuongezea tu kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi, barabara hii wakati bado ipo kwa TARURA ilikuwa imetengewa shilingi milioni 500 na Road Board kwa ajili ya matengenezo yake. Sasa baada ya kupandishwa hadhi fedha ile itahamia kwa wenzetu wa TANROADS ambapo bado watatekeleza kwenye barabara hii hii shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili ya Barabara ya Haporoto – Ileya – Ishinda. Barabara hii ina urefu wa kilometa tisa na kweli nikiri kwamba kwa sasa hali yake si nzuri sana. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 ambao tunauanza mwezi unaofuata, tayari barabara hii imetengewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuweza kutengeneza yale maeneo korofi kwa kumwaga changarawe na kuhakikisha kwamba inapitika vizuri, kwa sababu inaelekea katika eneo ambalo lina machimbo. Kwa hiyo nimtoe hofu Mheshimiwa Njeza, kwamba muda si mrefu ataona utekelezaji wa matengenezo ya barabara hii kwa hizi kilometa tisa.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali na yanatia matumaini kwa wananchi, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; mradi huu ulitegemewa kuwapatia umeme wa vijiji wanaopitiwa na mradi huu ikiwemo Vijiji vya Wambishe, Ihango katika Kata ya Ulenje na Vijiji vya Rusungomina katika Kata ya Iwindi na Bonde la Songwe ambako kuna viwanda vikubwa sana vinavyohitaji umeme mkubwa kwa ajili ya kuchakata madini. Sasa je, ni lini hawa wananchi watapatiwa umeme kwa mradi mbadala baada ya kuona huu mradi unasuasua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vilevile mradi wa REA III, awamu ya pili na mradi wa Densification umechelewa kwa kiasi kikubwa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kunusuru hii miradi miwili ambayo ukiangalia mradi wa densification umepitwa na wakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa kuendelea kufatilia mradi huu mkubwa tunaouita TAZA wa kupeleka umeme mkubwa katika maeneo hayo. Nimhakikishie tu kwa kauli ya Serikali kwamba mradi huu hausuisui, lakini ni taratibu za kimanunuzi zinazofanya mradi uonekane unachukua muda. Hata hivyo, kama tulivyosema kwenye jibu la msingi tayari taratibu za kufanya fidia zimekaribia kukamilika na kwenye mwaka wa fedha ujao tunatarajia kuanza kufanya fidia. Tayari wafadhili wameshapatikana na fedha ipo na ni taratibu za kukamilisha maandalizi ya utekelezaji wa mradi zinazoendelea na zitakapokamilika mradi utaanza mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee kwamba tayari vijiji hivyo alivyovitaja katika maeneo hayo viko katika program ya kupewa umeme na mradi huu. Tunayo program inayoitwa Land End Connection ambayo tunawaunganisha watu kwenye maeneo ya miradi mikubwa inapopita kama ambavyo wale wenzetu wanaopitiwa na mradi unaotoka Iringa kupita Dodoma, kupita Arusha kwenda Namanga walivyoona tukifanya kwenye maeneo hayo na huku pia tutafanya hivyo hivyo. Kwa hiyo niwaombe tu wananchi wa maeneo hayo wawe na matumaini na Serikali itawapelekea umeme katika maeneo yao baada ya kukamilisha taratibu za mradi ambao unatarajiwa kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, kuhusiana na REA ni kweli REA kama alivyosema siku chache zilizopita Mheshimiwa Waziri alipokuwa akijibu swali tulipata changamoto ya mabadiliko ya bei, lakini suala hilo tumelichukua kwa uzito wake kwa kukaa na wakandarasi na kukubaliana bei mpya zenye uhalisia kwa ajili ya kuendelea na utekelezaji wa mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya hayo, miradi hiyo katika maeneo mbalimbali inaendelea kwa hatua mbalimbali ya uthamini wa maeneo, ya kusimika nguzo, ya kuvuta nyaya kwa wale ambao walishapata vifaa hivyo kwa ajili ya utekelezaji. Kwa hiyo niwaonye, kuwaasa, kuwaomba, kuwashawishi na kuwashauri wakandarasi wote waendelee na utekeleaji wa miradi hii kwenye maeneo yao kwa sababu mikataba yetu ipo pale pale ili kuweza kufikisha azma yetu ya kukamilisha vijiji vyote vilivyobakia kwa wakati.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana; kwa kuwa wananchi wa Wilaya ya Mbeya, Jimbo la Mbeya Vijijini wameweza kujenga Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mbalizi na sasa kuna mahitaji makubwa ya kujenga kituo katika Kata ya Igoma na Kata ya Ilembo. Je, ni lini Serikali itaunga mkono nguvu za wananchi kwa ujenzi wa vituo hivyo viwili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali mawili ya Mheshimiwa Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuwapongeze wananchi wa kata hizo mbili ambao wameanza ujenzi wa vituo vya polisi vya kata zao, naomba nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara itatuma wataalam kutoka Jeshi la Polisi kwa ajili ya kufanya tathimini kuona kiwango cha ujenzi kilichofikiwa, kiasi gani cha fedha kinahitajika ili kumalizia tuweze kuingiza kwenye mpango wetu wa bajeti wa kumalizia vituo ambavyo vimejengwa kwa nguvu za wananchi. Kwa hiyo, tunaomba awe na subira kidogo.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa na mimi ningependa kujua je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi - Mkwajuni - Makongorosi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja tayari ipo kwenye ukamilishwaji wa kufanyiwa usanifu wa kina na baada ya hapo Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami ili kuiunganisha Mkoa wa Mbeya kwa maana ya Wilaya ya Mbeya na Wilaya ya Songwe kwa Mkoa wa Songwe, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, katika Mji wa Mbalizi, kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais wa kujenga barabara za mitaa kwa kiwango cha lami; je, ni lini barabara hizo zitajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo katika mchakato wa kutafuta fedha, na mara utakapopata fedha hizo maana yake tutaanza ujenzi ili kukamilisha ahadi za viongozi.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi, iliyoko Wilaya ya Mbeya yenye watu zaidi ya laki moja iliishapita vigezo vyote vya vikao vyote vya DCC, RCC na hata kiuchumi iko vizuri. Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi itapanda kuwa Halmashauri ya Mji?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, aliagiza hata kubadili Jina la Jimbo la Mbeya Vijijini. Je, ni lini Serikali itabadili jina la Jimbo la Mbeya Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji Mdogo wa Mbalizi ni kweli kwamba ni mamlaka ya Mji ya muda mrefu lakini tayari imeshafikisha vigezo kwa maana ya idadi ya watu, uwezo wa kiuchumi, lakini wameshafuata taratibu na kuwasilisha ofisi ya Rais TAMISEMI. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI sasa tunafanya tathmini lakini pia tunatambua vigezo hivyo na baadaye tutatawakilisha kwa mamlaka husika ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa kadri itakavyokuwa inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na jina la Halmashauri ya Jimbo la Mbeya Vijijini kubadilishwa ni taratibu ambazo zinafanywa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, kwa hivyo Ofisi ya Rais – TAMISEMI tumechkua hili tutashirikiana na Wizara husika kuona uwezekano wa kutekeleza maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, na mimi nilitaka kujua ni lini Serikali itatatua mgogoro kati ya Hifadhi ya Kitulo na wananchi wa Kijiji cha Kikondo, Kata ya Ilungu ambao ni
wa muda mrefu na viongozi wetu wa kitaifa walishatoa ahadi ya kutatua huo mgogoro na kisha wananchi walipwe fidia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Hifadhi ya Kitulo ina changamoto, kuna migogoro kati ya hifadhi na maeneo ya wananchi, lakini zoezi hili liliingizwa kwenye Kamati ya Mawaziri Nane na hivi ninavyoongea baada ya Bunge hili kuisha, zoezi hili litaendelea kwenda kutoa ufafanuzi katika maeneo yaliyobaki ikiwemo Mkoa wa Iringa na Njombe ambapo kamati hii haijafika. Hivyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hili tunaenda kulitekeleza, tutaenda kutatua migogoro hii na wananchi waweze kuishi kwa amani.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa majibu mazuri sana na pia kwa mikakati mizuri kuhakikisha eneo hili linatumika kiuchumi kwa nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile hili eneo liko mkabala na TAZARA na uwanja wa kimkakati wa Songwe na barabara ya TANZAM, je, Serikali ina mpango gani wa kutenga eneo kwa ajili ya bandari kavu na kujenga bandari kavu katika eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya umuhimu wa eneo hilo, je, ni lini Serikali itaanza upimaji na kutenga maeneo ya eneo hili muhimu?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kweli Mkoa wa Mbeya ni moja ya mikoa ya kimkakati ambayo Serikali inauangalia kuhakikisha unawekezwa vizuri, kwa maana ya miundombinu wezeshi. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, ni kweli eneo hili ni la kimkakati kwa sababu linapitiwa na barabara kuu inayoenda Zambia. Pia, kuna uwanja wa ndege na reli ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya maeneo ambayo Serikali inaweka mkazo ni kuweka miundombinu wezeshi yote. Hili suala la bandari kavu ambalo litasaidiana na miundombinu hii mingine nalo ni moja ya maeneo ambayo tunayaangalia ili kuboresha eneo hili ili liwe sehemu ya kusaidia kukuza biashara, kuuza nje lakini pia kuingiza bidhaa ambazo zinatoka maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tunasema eneo hili ni kwa ajili ya uwekezaji mauzo nje kwa sababu tunategemea baada ya miundombinu kukamilika na bandari kavu pia itasaidia kuuza nje, kwa maana ya kuuza bidhaa zinazozalishwa katika eneo lile kwenda nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upimaji, katika bajeti hii inayokuja tunayoenda nayo ni moja ya maeneo maalum ambayo tutaangalia namna ya kuyapima ili yaweze kutumika kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na miundombinu mingine ikiwemo bandari kavu katika eneo hili la Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.