Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Joseph Osmund Mbilinyi (4 total)

MHE. CATHERINE V. MAGIGE (K.n.y. MHE. JOSEPH O. MBILINYI) aliuliza:-
Je, ni lini jengo la maabara ya mionzi linalojengwa kwa muda mrefu sasa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mbeya litakamilika na vipimo vya CT-Scan na MRI-Scan vitaletwa na kuanza kazi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, niruhusu nitumie Bunge lako Tukufu kuwatakia kheri watoto wote wa Tanzania, watoto wote wa Afrika kwa kuwa leo ni siku ya Mtoto wa Afrika. Kaulimbiu ya mwaka huu tunasema „Ubakaji na Ulawiti kwa Watoto Vinaepukika, Chukua Hatua Kuwalinda Watoto‟.
Mheshimiwa Naibu Spika, Nataka kuwathibitishia watoto wa Tanzania kwamba Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha wabakaji na walawiti wa watoto wanafikiwa na mkono wa dola na kila mbakaji ajiandae kutumikia kifungo cha miaka 30. Tutawalinda watoto wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuwahamasisha wazazi, walezi, kuongeza jitihada za kuwalinda watoto wetu kwa sababu 48% ya ubakaji na ulawiti unatokea katika nyumba zetu. Kwa hiyo, nyumba zetu siyo salama kwa watoto wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya ilianza mradi wa ujenzi wa jengo…
NAIBU SPIKA: Mbeya Mjini, Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ilianza mradi wa ujenzi wa Jengo la X-Ray katika Hospitali ya Rufaa Mbeya tarehe 9 Novemba, 2010 lengo likiwa ni kuboresha huduma za uchunguzi katika hospitali hii inayohudumia wakazi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2013/2014 hadi 2014/2015 kiasi cha Sh.614,670,000/= kilitolewa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi katika mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2015/2016 kiasi cha shilingi bilioni 8 kilitengwa, fedha ambayo mpaka sasa haijatolewa. Hata hivyo, Wizara bado ina nia ya kukamilisha ujenzi wa mradi huu, hivyo katika mwaka wa fedha 2016/2017 Wizara imetenga kiasi cha shilingi bilioni 5 katika bajeti ya maendeleo ambazo zitatumika kama ifuatavyo:-
(i) Shilingi bilioni 3 zitatumika kuendeleza ujenzi pamoja na kulipa deni lililobaki kwa mkandarasi aliyekuwa anajenga; na
(ii) Shilingi bilioni 2 zitatumika kununua vifaa tiba zikiwemo CT-Scan na MRI.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni matarajio yangu kwamba ujenzi huu utakamilika mwaka ujao wa fedha 2016/2017 pamoja na kusimika vifaa.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI aliuliza:-
Kumekuwa na tabia za watu kupiga watu wengine hovyo kila siku, vipigo hivyo vinafikia kiasi cha utesaji (torture) kama ilivyotokea Mbeya Sekondari kwa walimu kumshambulia mwanafunzi au mtu kumtoa macho kama ilivyotokea huko Buguruni na maeneo mengine:-
(a) Je, Serikali inaona mateso haya wanayopata Watanzania kutoka kwa Watanzania wenzao?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani ili kuwalinda wananchi na vitendo hivi vya kikatili?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hivi karibuni kumekuwepo na vitendo vya kusikitisha katika nchi yetu na kwa jamii ambavyo ni kinyume cha sheria na havikubaliki. Aidha, Serikali haikubaliani na vitendo vya namna hii vinavyofanywa na mtu/watu/ kikundi kwani vitendo hivyo ni kinyume na sheria na utaratibu mzima wa haki za binadamu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ili kuzuia na kuwalinda raia na mali zao. Aidha, Serikali kupitia Jeshi la Polisi hupokea taarifa za matukio mbalimbali na kuyafanyia uchunguzi wa kina na inapobainika upo ushahidi wa kutosha, mtuhumiwa huchukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria. Nichukue fursa hii kuwaasa sana wale wote ambao wanakiuka taratibu, kanuni na sheria za nchi waache tabia hiyo mara moja. Wizara yangu haitakuwa na suluhu na mtu yeyote atakayetenda uhalifu huo.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI aliuliza:-
Nyumba nyingi katika barabara kuu ya Zambia Jijini Mbeya kuanzia maeneo ya Uyole mpaka Lwambi ziliwekwa alama ya “X” kuashiria kuvunjwa ili kupisha upanuzi wa barabara hiyo muhimu na wapo wananchi waliowekewa alama nyekundu walivunja nyumba zao wenyewe na
wananchi waliowekewa alama ya “X” za kijani bado wanasubiri fidia.
(a) Je, mradi huo umefikia wapi na ni lini upanuzi huo utaanza?
(b) Je, upanuzi huo umezingatia ushauri wangu wa kuweka njia nne (four lines) toka Uyole mpaka Songwe Airport ili kuondoa kabisa tatizo la foleni ambalo linakua siku hadi siku Jijini Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekaji wa alama za ‘X’ katika majengo yaliyopo ndani ya hifadhi ya barabara kuu ya TANZAM Jijini Mbeya pamoja na maeneo mengine mengi nchini ni utekelezaji wa Sheria ya Barabara Na. 13 ya mwaka 2007 na kanuni zake za mwaka 2013. Kutokana na sheria hiyo, mapendekezo yote yaliyopo ndani ya mita 22.5 kutoka katikati ya barabara kwenda kila upande yanapaswa kuondolewa bila fidia, hivyo wamiliki wote wa mali zilizokuwepo ndani ya eneo hilo waliwekewa alama za ‘X’ nyekundu na kupewa notice za kubomoa nyumba zao bila fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wote waliokuwa na maendelezo kati ya mita 22.5 na mita 30 kutoka katikati ya barabara kila upande wa barabara, kabla Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 haijaanza kutumika waliwekewa alama za ‘X’ za kijani na kupewa notice za kutofanya
maendelezo mapya kwa kuwa maendelezo yaliyopo yatalipwa fidia wakati eneo hilo litakapohitajika kwa ajili ya upanuzi wa barabara ili kujiweka tayari na kuzuia ucheleweshaji wa kuanza kazi za ujenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upanuzi wa barabara ya kutoka Mbeya kwenda Zambia hususan kuanzia Uyole kwenda Songwe utaanza pale upembuzi yakinifu na usanifu wa kina utakapokamilika na kuonesha viwango vya upanuzi vinavyohitajika na Serikali tutakapopata fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali inakusudia kujenga barabara ya mchepuo wa Mbeya (Mbeya Bypass) yenye urefu wa kilometa 40 inayoanzia Uyole hadi Songwe ambapo mradi huu upo kwenye hatua ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na unatekelezwa chini ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua sahihi ya kuondoa msongamano na magari kwenye Jiji la Mbeya itatokana na mapendekezo yatakayotolewa baada ya kukamilika kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina unaoendelea.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI aliuliza:-

Katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Wizara ya Afya iliomba na kutengewa shilingi bilioni tano kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo la maabara na ununuzi wa vipimo vya kisasa kama CT Scan na MRI Scan katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya.

(a) Je, ni kiasi gani cha fedha kimeshatolewa mpaka sasa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi huo?

(b) Kwa kuwa bajeti inayohitajika imeshatengwa; je, ni lini ujenzi huo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilipeleka shilingi bilioni moja, na baadaye katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto iliomba na kuidhinishiwa jumla ya shilingi bilioni tano kwa ajili ya ukamilishaji ujenzi wa jengo la huduma za radiolojia na ujenzi wa Jengo la Wazazi Meta katika Hospitali ya Kanda ya Rufaa Mbeya. Hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni tatu zimeshapokelewa kwa ajili ya kazi hizo ambapo shilingi bilioni mbili ni kwa ajili ya kumalizia mradi wa ujenzi wa jengo la radiolojia na ununuzi wa baadhi ya vifaa vya radiolojia na bilioni moja kwa ajli ya kugharamia ujenzi wa jengo la wazazi katika Hospitali ya Rufaa Meta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi umeshakamilika kwa asilimia 90 na kwa sasa mafundi wanakamilisha kuingiza umeme katika jengo baadhi ya ununuzi wa transofoma. Hivyo, hadi kufikia mwezi Machi 2019 jengo litakuwa limekamilika rasmi. Aidha, Serikali tayari imeshanunua CT- Scan kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ambayo inasubiria kukamilika kwa jengo maalum ili iweze kusimikwa rasmi. Vilevile hospitali hii inategemea kupatiwa mashine ya MRI kupitia Mradi wa ORIO wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Taratibu za manunuzi wa vifaa hivi unaendelea.