Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Victor Kilasile Mwambalaswa (1 total)

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
La kwanza, sheria hiyo katika marekebisho hayo, ukija upande wa mazao ya tumbaku, iliondoa chama kikuu cha APEX cha Morogoro kwenye ushirika wa tumbaku. Baada ya kuiondoa hiyo APEX ina maana hata ile tozo ya asilimia tano ambayo APEX ilikuwa inachukua kwenye bei ya mkulima, ipo. Je, hiyo tozo sasa itarudi kwenye vyama vya msingi vya wakulima au inafanya nini?
Mheshimiwa Spika, la pili, Vyama vya Msingi vinapotaka kukopa pembejeo za zao lao vinapitia kwenye Vyama vya Ushirika vya Wilaya kwenda kwenye mabenki. Vikipitia kwenye Vyama vya Ushirika vya Wilaya kwenda kupata mkopo huo, kunakua na gharama ambapo Chama cha Ushirika cha Wilaya kinakitoza chama cha msingi, kinasema ni kwa sababu ya utawala. Je, lini Serikali sasa itatengeneza kanuni ambayo itakifanya chama cha msingi chenyewe ndiyo kiende kukopa benki pembejeo hizo?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Naibu waziri kwa majibu mazuri.
Kuhusu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimwa Mwambalaswa, niseme tu kwamba Serikali inapanga kuyapitia upya makato yote yanayokwenda kwenye mazao, zikiwepo tozo zote hizo zinazotolewa; na pia inapanga kuangalia upya mfumo wa ugawaji wa pembejeo kwa wakulima wa mazao haya ambayo ameyataja.
Mheshimiwa Spika, nategemea kuyatolea kauli ndani ya siku mbili hizi tutakapokuwa tunatolea majibu ya hoja za Wabunge kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Rais, kwa sababu tayari Mheshimiwa Rais alishaonesha kukerwa na tozo nyingi zinazowaangukia wakulima kwenye mazao haya. Vilevile wakati anazunguka kwenye kampeni alishawaahidi na sisi wasaidizi wake tunatembea kwenye maneno ya Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, tutatoa tamko kwa kuhakikisha kwamba wakulima wanaacha kubeba mzigo mzito wa makato hayo.