Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Eng. Hamad Yussuf Masauni (229 total)

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Kutokana na wizi wa mifugo uliokithiri katika Bonde la Yayeda Chini, Serikali ilianzisha kituo cha polisi na sasa kimeondolewa:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukirudisha kituo hicho ili wananchi wapate huduma za ulinzi wa mifugo na mali zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa kituo cha polisi cha Bonde la Mto Yayeda Chini kilianzishwa kutokana na matukio ya kukithiri kwa matukio ya wizi wa mifugo. Kufuatia hali hiyo, Jeshi la Polisi lilipeleka gari PT Na. 1008, Landrover kituo cha polisi cha Hydom kinachotoa huduma ya ulinzi wa eneo hilo na kuanzisha doria za mara kwa mara ili kupambana na wimbi la wizi wa mifugo. Kwa hivi sasa, hali ya wizi wa mifugo na uhalifu mwingine katika eneo hilo umepungua.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kituo hicho hakijaondolewa bali taratibu za kutoa huduma za ulinzi zimebadilika; ambapo askari hupangwa kwa kazi za ulinzi wa doria eneo hilo kwa kipindi maalum na kwa awamu. Jeshi la Polisi litaendelea kutathmini na kuzingatia hali ya uhalifu wa eneo hilo katika kutoa huduma stahiki za ulinzi na usalama.
MHE. DAVID E. SILINDE (K.n.y MHE. FRANK G. MWAKAJOKA) aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina Mpango gani wa kugenga Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Wilaya hapa Tunduma ili kuendana na ongezeko la watu na wageni wanaoingia nchini?
(b) Je, Serikali haioni vema ujenzi wa kituo hicho uende sambamba na ujenzi wa nyumba zenye gharama nafuu kwa Polisi wetu ambao wana shida kubwa ya makazi?
SPIKA: Sasa Mheshimiwa Silinde wewe Tunduma si ulishaondoka, majibu ya swali hilo Mheshimiwa Naibu, Waziri Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Hamad Yussuf Masauni. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI YA WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Kituo cha Polisi Tunduma ni kidogo na hakina nyumba za kutosha. Wilaya ya Momba inahitaji nyumba 150 ili kukidhi mahitaji ya makazi ya Askari. Kama ilivyo kwa maeneo mengi hapa nchini, changamoto kubwa ya ujenzi wa vituo vya Polisi na nyumba za askari ni uhaba wa fedha. Aidha, kwa Kituo cha Polisi Tunduma changamoto nyingine ni eneo la kufanya upanuzi wa kituo kilichopo sasa kwani kituo hicho kipo mpakani kando mwa barabara ya Sumbawanga.
Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha Jeshi la Polisi linaboreshewa makazi na kuwa na ofisi ili kuwezesha utoaji huduma kwa wananchi kuwa mzuri. Jeshi la Polisi chini ya utaratibu wa mikopo nafuu kutoka taasisi za kifedha za ndani na nje ya nchi lina mpango wa kujenga nyumba na ofisi za Polisi maeneo mbalimbali nchini. Kwa hivi sasa Serikali inakamilisha taratibu za kupata mkopo toka Bank ya Exim ya China ili kujenga nyumba 4,136 za makazi ya Askari katika Mikoa 17 hapa nchini.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Kwa miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya ujambazi unaohusiana na uporaji wa fedha na ni muhimu sana Watanzania wakapata ufahamu kwa takwimu kuhusu ukubwa au udogo wa tatizo hilo kuliko kupata taarifa ya tukio moja moja:-
(a) Je, ni zipi takwimu sahihi na mchanganuo wa matukio ya ujambazi unaohusiana na uporaji wa fedha ikiwa ni pamoja na vifo na majeruhi ya matukio hayo kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 Kitaifa?
(b) Je, ni mikoa gani miwili inayoongoza na mikoa gani miwili yenye matukio hayo machache?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya ujambazi yanayohusisha uporaji wa fedha kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 yalikuwa kama ifuatavyo:-
Mwaka 2013 matukio 1,266; mwaka 2014 matukio 1,127; na mwaka 2015 yalikuwa 913. Jumla ya matukio yalikuwa 3,306 yaliyosababisha jumla ya vifo vya watu 91 na majeruhi 189.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mikoa inayoongoza kwa matukio hayo katika kipindi hicho ni Dar es Salaam iliyokuwa na matukio 733, yaliyopelekea vifo vya watu 65 na majeruhi 43. Mkoa uliofuata ulikuwa ni Mara uliokuwa na matukio 375 ya uporaji yaliyosababisha vifo 11 na majeruhi sita. Aidha, Mkoa wa Kaskazini Pemba pamoja na Kusini Unguja haukuwa na matukio ya uporaji wa fedha kabisa.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Matukio ya wananchi kujichukulia sheria mkononi yamezidi kuongezeka siku hadi siku na kusababisha madhara na vifo kwa watu wasio na hatia:-
Je, Serikali inafanya juhudi gani ili kupunguza au kuondoa kabisa ukatili huu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo vya mtu ama watu kujichukulia sheria mikononi ni uhalifu ambao umeanza kushamiri katika jamii yetu ikiwemo Visiwa vya Zanzibar katika kipindi cha mwaka 2013/2014. Jumla ya matukio 2,041 yaliripotiwa katika vituo mbalimbali vya polisi nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013 kulikuwa na matukio 1,112 ambapo Zanzibar yaliripotiwa matukio 14. Mwaka 2014 yalipungua na kufikia matukio 929, kati ya hayo Zanzibar yalikuwa ni matukio matano. Aidha, matukio yote yalichukuliwa hatua stahiki ikiwemo wahusika kukamatwa na kufikishwa Mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi, limekuwa likichukua hatua mbalimbali za kupambana na wimbi la uhalifu huo, miongoni mwa juhudi hizo ni pamoja na kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa kufuata sheria. Aidha, Jeshi la Polisi huwakamata na kuwafikisha Mahakamani watu wanaojichukulia sheria mkononi, kutenda makosa mbalimbali ya jinai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu, kutoa rai kwa wananchi wote kujiepusha na vitendo vya kujichukulia sheria mkononi, naomba Waheshimiwa Wabunge wote kushirikiana na Serikali kuwaelimisha wananchi kuepuka vitendo hivyo.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-
Kwa kuwa barabara kuu kwenda mikoani zina foleni na tukiangalia barabara hizo zinatumika na magari mengi ya mizigo ambayo mara nyingi huwa ni chanzo cha ajali na Watanzania wengi kupoteza maisha:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha ajali hizo zinapungua?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyowahi kujibiwa swali la msingi namba 13, 74, 75 na 167, katika Mikutano mbalimbali ya Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zipo sababu nyingi za vyanzo vya ajali za barabarani nchini. Utafiti wa kisayansi unaonesha kuwa, sababu hizo zimegawanyika katika makundi makuu matatu:-
Kwanza, sababu za kibinadamu kama vile ulevi na uzembe zinazochangia asilimia 76 ya ajali zote.
Pili, ubovu wa vyombo vya usafiri zikiwemo hitilafu za kiufundi na mfumo wa umeme wa magari unaochangia asilimia 16.
Tatu, mazingira ya barabara yaani ubovu, ufinyu na usanifu mbaya wa barabara zetu unachangia asilimia saba tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kuwa, suala la msongamano wa magari ambao linahusiana zaidi na mazingira ya barabara linachangia kiasi kidogo cha ajali ikilinganishwa na sababu zingine nilizozitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajali nchini ni tatizo ambalo kutokana na madhara yake kwa umma, Serikali itaendelea kukabiliana nalo kwa nguvu zote. Kwa kuzingatia hali hii, Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani likishirikiana na wadau wengine wa usalama barabarani limechukua hatua zifuatazo:-
(1) Kusimamia kwa karibu mifumo ya sheria ukiwemo utaratibu mpya wa malipo ya papo kwa papo (notification) kwa njia ya kielektroniki ulioanzishwa hivi karibuni katika Jiji la Dar es Salaam na baadaye kutumika kwa nchi nzima.
(2) Kunyang‟anya leseni za madereva wazembe wanaorudia kutenda makosa ya usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kuwakamata na kuwafikisha Mahakamani pindi wanaposababisha ajali.
(3) Kuwafukuza au kuwabadilisha kazi Askari wa Usalama Barabarani wanaotuhumiwa kujihusisha katika vitendo vya rushwa ambavyo vimekuwa vikichochea ongezeko la ajali barabarani.
(4) Kutoa elimu na namba za simu za viongozi wa Kikosi cha Usalama Barabarani kwa wananchi ili wafahamu haki zao wanapokuwa abiria au watumiaji wa barabara na kutoa taarifa wanapotendewa isivyo halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwaagiza madereva na watumiaji wengine wa barabara kote nchini kuzingatia Sheria za Usalama Barabarani na kutoa taarifa za dereva, askari au mtu yoyote anayekiuka sheria za barabarani au taratibu za kazi kwa makusudi ili hatua stahiki zichukuliwe.
MHE. KISWAGA B. DESTERY aliuliza:-
Pamoja na kwamba polisi ni walinzi wa raia na mali zao, ila wanakabiliwa na changamoto za nyumba za kuishi, maslahi duni na ukosefu wa vitendea kazi:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha vitendea kazi kama magari na mafuta?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za askari polisi na kuboresha mishahara yao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga Boniventura Destery, Mbunge wa Magu lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiboresha hali ya vitendea kazi kwa Jeshi la Polisi ikiwemo vyombo vya usafiri, mawasiliano na zana nyingine za kazi. Mathalani kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ililipatia Jeshi la Polisi jumla ya magari 387 kati ya magari 777 yanayotarajiwa kununuliwa. Aidha, Serikali inatarajia kuongeza fedha ya mafuta na vilainishi katika bajeti ya mwaka wa fedha ya 2016/2017. Ni kweli kuwa Jeshi la Polisi, linakabiliwa na changamoto ya uhaba wa nyumba za makazi ya Askari. Kupitia Mpango Shirikishi wa wadau mbalimbali na mikopo yenye riba nafuu, Serikali inakusudia kujenga nyumba jumla yake ni kama 4,136 katika mikoa 15 pamoja na Mikoa mitano ya Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo la makazi kwa askari. Serikali inaandaa mpango mkakati wa kujenga nyumba zaidi ya 35,000 kufikia mwaka 2025, ikiwa ni wastani wa takriban nyumba 3,500 wa kila mwaka.
Aidha, Serikali itaendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kutatua changamoto za makazi ya askari kwa kudhamini mikopo nafuu kutoka Taasisi ya kifedha na kuchangia ujenzi wa nyumba pale bajeti inaporuhusu. Kama ilivyo kwa watumishi wengine wa Umma, Serikali imekuwa ikiongeza viwango vya mishahara, kwa Askari wa Jeshi la Polisi kila mwaka.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa Kituo cha Polisi Mkokotoni kilichoko Unguja?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Kituo cha Polisi Mkokotoni bado haujakamilika. Hadi sasa kazi ya ujenzi wa kituo hicho imefikia asilimia 80 ikihusisha ujenzi wa jengo lenyewe, kupauwa na kupigia plasta kuta zote. Kazi kubwa iliyobaki ni kufunga milango, madirisha, kuweka sakafu, kupiga rangi na kununua furniture. Serikali inakusudia kumalizia ujenzi wa kituo hicho ndani ya mwaka wa fedha 2016/2017 kulingana na upatikanaji wa fedha za bajeti.
MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-
Yamekuwepo malalamiko mengi ya kuongezeka kwa vitendo vya uhalifu wa kupiga watu, kuwatesa, kuchoma mali na kutishia amani katika Kisiwa cha Unguja Wilaya za Magharibi na Mjini na kwamba wahusika wamekuwa hawajulikani:-
(a) Je, ni kwanini hali hiyo imeachwa kuendelea kwa muda mrefu?
(b) Je, ni kwa nini Jeshi la Polisi limeshindwa kuwakamata wahusika?
(c) Je, wananchi hao wategemee lini vitendo hivyo kutoweka?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwepo na ongezeko la matukio saba ya uhalifu katika Wilaya ya Magharibi na Mjini kwa mwaka 2015 ambapo jumla ya matukio 139 yaliripotiwa katika Vituo vya Polisi ikilinganishwa matukio 132 ya mwaka 2014. Hata hivyo pamoja na kuwepo kwa ongezeko hilo takwimu zinaonesha kuwa vitendo hivyo vya makosa ya jinai kwa ujumla Visiwani Zanzibar vinapungua kwa kasi ya kuridhisha. Mathalani, kwa mwaka 2015 jumla ya makosa 1,673 ya jinai yaliripotiwa katika Kituo cha Polisi, ikilinganishwa na makosa 3,227 yaliyoripotiwa mwaka 2014. Hii ni pungufu ya makosa 1,554, sawa na wastani wa asilimia 51.8.
Mheshimiwa Naibu Spika, vitendo vya uhalifu Zanzibar havijafumbiwa macho hata kidogo kama inavyodhaniwa na baadhi ya watu, kwani kutokana na takwimu zilizoainishwa awali, ni dhahiri kuwa uhalifu Zanzibar sio tu wa kutisha na unaendelea kudhibitiwa. Jeshi la Polisi linao wataalam wa kupambana na wahalifu wa aina mbalimbali na litaendelea kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wale wote wanaovunja sheria.
MHE. MGENI JADI KADIKA aliuliza:-
Kwa muda mrefu walemavu wa ngozi (albino) wamekuwa wakiishi kwa hofu katika nchi yao kutokana na kuuawa na kukatwa viungo vyao kwa imani za kishirikina ikiwemo kwa ajili ya kushinda uchaguzi au kujipatia mali:-
Je, Serikali ina mpango wa kuwalinda na kuwahakikishia usalama wa maisha yao watu hao wenye ulemavu wa ngozi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyowahi kujibiwa katika swali la msingi namba 99 na swali namba 60 katika mikutano tofauti ya Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu usalama wa ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi, Serikali kupitia Jeshi la Polisi na wadau wengine imekuwa ikichukua hatua za maksudi kukomesha mauaji hayo ikiwa ni pamoja na kuwasaka na kuwakamata watuhumiwa pamoja na kuwafikisha mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya pia juhudi za kuanzisha vituo vya kuwahudumia watu wenye ulemavu wa ngozi ambavyo vimesaidia kuimarisha ulinzi. Pia Jeshi la Polisi kwa kutumia falsafa ya Polisi Jamii inatoa elimu kwa umma juu ya madhara ya vitendo vya ukatili na mauaji na kujerui yanayofanywa na baadhi ya watu kwa msukumo wa imani potofu ya ushirikina. Aidha, Jeshi la Polisi limekuwa likifanya operesheni maalum za mara kwa mara zikiwamo za kukamata waganga wa jadi wanaopiga ramli chonganishi ambazo ni kichocheo kikubwa cha ukatili dhidi ya walemavu wa ngozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Jeshi la Polisi ikishirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama za Vijiji, Kata, Wilaya na Mikoa imeanzisha vikosi kazi hususan kwenye Mikoa na Wilaya zilizojitokeza kukithiri kwa matukio haya ili kuratibu na kusimamia kwa karibu ulinzi wa ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi. Vikosikazi hivyo hufanya kazi kwa kukusanya taarifa za kiintelejensia na kuzifanyia kazi.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR aliulliza:-
Bunge la Jamhuri ya Muungano hupitisha Bajeti ya Serikali kwa kila Wizara kwa mwaka ikiwemo Wizara ya Mambo ya Ndani:-
(a) Je, inakuwaje Wilaya yenye vituo saba vya polisi ina gari moja tu na inapatiwa lita tano hadi saba tu za mafuta kwa siku?
(b) Je, Serikali iko tayari kuziongezea mafuta na magari Wilaya za Magharibi A na B zenye vituo vya polisi vya Fumba, Mbweni, Mazizini, Mwanakwerekwe, Kijitoupele, Fuoni, Airport na Mfenesini ambazo ni gari moja tu kila Wilaya ili kukongeza ufanisi na kuendana na kasi ya hapa kazi tu hasa ukizingatia kuwa Zanzibar inajiandaa na marudio ya Uchaguzi Mkuu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir, Mbunge wa Dimani lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa Wilaya ya Magharibi A na B hazina magari na mafuta ya kutosha kwa shughuli za polisi. Hali hii ni changamoto kwa vituo vingi vya polisi hapa nchini, hata hivyo, mgawo wa vitendea kazi yakiwemo magari huzingatia jiografia ya Wilaya. Hali ya uhalifu na idadi ya watu wanaohudumiwa na kituo husika na siyo idadi ya vituo vidogo vya Polisi vilivyopo katika Wilaya husika.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, inakusudia kuwasilisha bajeti mbele ya Bunge lako Tukufu ili kuboresha hali ya vyombo vya usafiri, mafuta na vilainishi ili kukidhi mahitaji halisi ya Jeshi la Polisi hapa nchini, vikiwemo Vituo vya Polisi alivyovitaja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. USSI SALUM PONDEZA AMJAD aliuliza:-
Kituo cha Polisi Maruhubi kinakabiliwa na matatizo mbalimbali kama vile ukosefu wa askari wa kutosha; kituo hakitoi huduma saa 24, lakini pia majengo yake ni machakavu sana kiasi kwamba hayana hadhi ya kuwa Kituo cha Polisi:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka askari wa kutosha katika kituo hicho na kuhakikisha kuwa kituo kinatoa huduma zake kwa saa 24?
(b) Je, ni lini Serikali itayakarabati majengo ya kituo hicho ili yaendane na hadhi ya Kituo cha Polisi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi cha Maruhubi ni Kituo cha Daraja “C” ambacho taratibu za utoaji huduma kwa mujibu wa miongozo ya Jeshi la Polisi kitatoa huduma kuanzia saa 12.00 asubuhi hadi saa 12.00 jioni na kuwa na askari wasiozidi 20.
(b) Mheshimiwa Spika, Serikali itakifanyia ukarabati Kituo cha Maruhubi mara tu fedha zitakapopatikana.
MHE. JOHN P. KADUTU (k.n.y. MHE. RICHARD P. MBOGO) aliuliza:-
Mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1992 na wengine waliozaliana katika makambi ya wakimbizi ya Katumba, Mushamo na Ulyankulu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kuwapa wakimbizi waliosalia?
(b) Ili kuondoa hali ya sintofahamu katika Sheria ya Wakimbizi Na. 20 inayokataza mikusanyiko zaidi ya watu watano, je, ni lini Serikali itafuta hadhi ya makambi ya wakimbizi katika maeneo ya Katumba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, napenda kurekebisha swali hilo kwamba ni kweli mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1972 na siyo mwaka 1992. Pia hakuna Sheria ya Wakimbizi Na. 20 bali ipo Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998. Vilevile maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge ni makazi ya wakimbizi na siyo makambi ya wakimbizi na hakuna mkimbizi aliyepo kambini aliyepewa uraia.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kushughulikia Wakimbizi (UNHCR) ipo katika hatua za mwisho kufanya uhakiki kamili kwa wakimbizi walengwa ili kutoa uraia kwa wanaostahili, kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi. Tunategemea hadi kufikia mwisho wa mwaka huu kazi hii itakuwa imekamilika ili taratibu za kutoa uraia kwa mujibu wa sheria ziweze kufanyika.
Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 20 cha Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998 kinahusu wakimbizi na hasa kililengwa kwa wakimbizi waliopo makambini katika makazi ya Katumba, Ulyankulu na Mishamo. Wengi wa wakazi wake sasa ni raia, sio wakimbizi. Kwa hiyo, kifungu hicho hakiwahusu kwa kuwa sasa wakazi wengi wa Katumba, Ulyankulu na Mishamo wameshapewa uraia. Wizara yangu kwa kushirikiana na TAMISEMI inaandaa utaratibu wa kufuta utengefu wa maeneo haya ili viwe vijiji vya kawaida kwa mujibu wa sheria.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR (K.n.y. MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO) aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kunusuru mauaji ya vikongwe nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeweka mikakati mbalimbali ya kunusuru mauaji ya vikongwe nchini ikiwa ni pamoja na:-
(i) Kufanya operesheni na misako ya mara kwa mara kubaini waganga wa jadi wanaojihusisha na upigaji ramli chonganishi na wasiofuata sheria;
(ii) Kutoa elimu kupitia Polisi Jamii, wadau mbalimbali wa ulinzi na usalama, madhehebu ya dini na mashirika na taasisi binafsi, lengo likiwa ni kuwaelimisha wananchi madhara ya kujichukulia sheria mkononi; na
(iii) Kuanzishwa kwa vikosi kazi ili kuweza kufuatilia na kutafuta taarifa mbalimbali za watuhumiwa wanaotenda matukio hayo maarufu kama wakata mapanga, kabla na baada ya kufanyika kwa tukio.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kwenye Bunge lako Tukufu kutoa rai kwa wananchi kuacha vitendo vya kujichukulia sheria mkononi vinavyosababisha mauaji kwa nchi yetu inaendeshwa kwa mujibu wa sheria.
MHE. ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Kituo cha Polisi cha Marine Kipili, hakina usafiri wa nchi kavu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakisaidia kitu hicho usafiri wa nchi kavu angalau hata kukipatia pikipiki?
(b) Je, ni lini Serikali itaongeza mgao wa petroli?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally KeissyMohamed, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi Karibuni Serikali imegawa vyombo vya usafiri takribani kwa Wilaya zote, ikiwemo Wilaya ya Nkasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Kipili kimo ndani ya Wilaya ya Nkasi kikihudumiwa na gari Namba PT 3836 ambayo ni jipya lililotolewa hivi karibuni. Hata hivyo, utaratibu utafanyika ili wapewe pikipiki iweze kusaidia kupunguza tatizo la usafiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaongeza mgawo wa mafuta kulingana na hali ya uchumi itakavyoimarika.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi wa kuwadhibiti wakimbizi hasa maaskari ambao hutoroka kambini Nduta na kwenda kujumuika na wananchi, hivyo kuhatarisha usalama wa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Atashasta Nditiye, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika, nchi yetu imekuwa ikipokea wakimbizi kwa miaka mingi na kuwahifadhi katika Kambi na Makazi. Kwa mujibu wa Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998 kifungu cha 16 na 17 kinaelekeza kuwa wakimbizi wote wanaishi katika maeneo maalum yaliyotengwa kwa ajili yao na hawaruhusiwi kutoka bila kibali maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kudhibiti wakimbizi hasa maaskari kutoka nje ya kambi, Serikali imejiwekea mikakati ya makusudi ikiwemo kuwagundua wakimbizi/askari kwa kuwafanyia usaili wa awali na wale watakaobainika hupelekwa katika Kituo cha Utenganisho cha Mwisa kilichopo mkoani Kagera ambako huwekwa chini ya uangalizi kwa kipindi cha miezi mitatu hadi sita.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Serikali kujiridhisha na mienendo yao, hutakiwa kukana uaskari na kuomba hifadhi upya kwa masharti ya kutokujihusisha na harakati zozote za kisiasa na kijeshi zilizopo nchini. Hata hivyo Ofisi za Wakuu wa Kambi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi hukusanya taarifa za kiintelejensia na kufanya doria na misako mara kwa mara kambini na nje ya kambi ili kubaini wakimbizi watoro na wanapobainika hushtakiwa na kuadhibiwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakimbizi.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Baadhi ya Kambi za Jeshi la Wananchi nchini (JWTZ) zina majengo chakavu sana ikiwemo Kambi ya Nyuki Zanzibar:-
Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa Kambi hizi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Msabaha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Kambi za Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania zina majengo chakavu ikiwemo Kambi ya Nyuki, Zanzibar. Hali hii imetokana na ukweli kwamba, Kambi nyingi za Jeshi zilirithi majengo yaliyokuwa yanatumiwa na Taasisi nyingine. Hata hivyo, Jeshi lina utaratibu wa kufanyia matengenezo majengo yake mara kwa mara kwa kadri ya upatikanaji wa fedha za bajeti za maendeleo.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED aliuliza:-
Je, Serikali imefanikiwa kwa kiasi gani kuimarisha majengo na vituo vya Polisi sanjari na kulipa madeni ya Wakandarasi waliojenga majengo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Ali Mohammed, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uchakavu na uhaba wa majengo ya ofisi za Polisi pamoja na nyumba za makazi kwa Askari. Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kukarabati ofisi na vituo vya Polisi na kujenga nyumba za kuishi Askari. Mathalani, mwaka 2012 Serikali ilijenga maghorofa 15, katika maeneo ya Buyekela Mkoa wa Kagera, matatu yenye uwezo wa kuchukua familia 12. Mkoa wa Mwanza Mabatini sita yenye uwezo wa uchukua familia 24 na Mkoa wa Mara Musoma sita yenye uwezo wa kuchukua familia 24.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiwalipa Wakandarasi wa miradi ya ujenzi wa ofisi na makazi ya Askari kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha za maendeleo. Mathalani katika mwaka wa fedha wa 2016/2017 Serikali imetenga kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni tano kwa ajili ya maendeleo.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-
Katika Jimbo la Tumbatu kumekuwa na matukio ya uvunjifu wa amani kwa wananchi wanaoishi katika kisiwa hicho na katika hali ya namna hiyo inaporipotiwa kwa Jeshi la Polisi inakuwa tabu kwenda kwa haraka kwenye eneo husika kwa sababu kadhaa ikiwemo ya ukosefu wa usafiri:-
Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga Kituo cha Polisi katika kisiwa hicho na kuwapatia usafiri wa uhakika kwa kuzingatia jiografia ya maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo matukio ya kihalifu yanayoripotiwa kutokea katika Kisiwa cha Tumbatu. Jeshi la Polisi linafanya jitihada za kukabiliana na uhalifu kwa kutoa huduma za ulinzi na usalama katika maeneo ya Kisiwa cha Tumbatu kwa kila siku kuwapeleka Askari wa doria ili kuimarisha ulinzi. Kwa sasa lipo boti lenye uwezo wa kubeba Askari 10, iwapo uwezo wa kifedha ukiongezeka hitaji letu ni kupata boti kubwa la mwendo kasi lenye uwezo wa kubeba Askari zaidi ya 10.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona haja ya kuwepo Kituo cha Polisi katika eneo hilo, ili kusogeza huduma za ulinzi na usalama na hali halisi ya kisiwa hicho kilichozungukwa na bahari na uwepo wa matukio ya uhalifu. Katika kutekeleza hilo tayari Serikali imepata kiwanja na makisio ya ujenzi wa kituo hicho yanaendelea. Aidha, Serikali kupitia Bunge lako Tukufu inapenda kuhamasisha wadau werevu na wananchi, akiwemo Mheshimiwa Mbunge, kutoa msaada wa hali na mali katika ujenzi wa kituo hiki.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR (K.n.y MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOSS NYIMBO) aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka uzio kwenye vituo vikubwa vya Polisi vilivyopo Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Galloss, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inao mpango wa kujenga uzio katika Vituo na Makambi yote ya Polisi Tanzania. Aidha, Jeshi la Polisi kwa kutumia rasilimali zilizopo eneo husika, limekuwa likijenga uzio wa muda au wa kudumu katika maeneo mbalimbali na litaendelea kujenga uzio katika vituo zaidi hatua kwa hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Zanzibar, Serikali imeanza kujenga uzio kwa baadhi ya maeneo ya Kambi ya Ziwani Zanzibar, mathalani eneo la Chuo Ujenzi umeanza kwa kutumia fedha zilizotokana na mapato ya ndani. Aidha, kwa upande wa mbele ujenzi unafanyika sambamba na kujenga maduka ambayo yatasaidia kuendesha shughuli za Polisi na kujiingizia mapato.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Makazi ya askari yamekuwa ya zamani pia mengine yamekuwa mabovu sana, mfano nyumba za Ziwani Zanzibar, Wete, Pemba na Chakechake Pemba hazikaliki kabisa.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuzifanyia marekebisho nyumba hizo?
(b) Je, ni gharama gani Serikali itatumia kwa marekebisho ya nyumba hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo lenye sehemu (a), na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nyumba nyingi za makazi ya askari hazijafanyiwa ukarabati zikiwemo za Ziwani Zanzibar, Wete na Chakechake. Serikali ina mpango wa kuzifanyia marekebisho nyumba zote za polisi Unguja na Pemba kwa kadri uwezo wa fedha utakavyoongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama halisi za ukarabati wa nyumba zote za polisi Unguja na Pemba ni bilioni 1.5.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza:-
Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la makazi kwa askari wa Jeshi la Polisi na Mheshimiwa Rais aligusia azma hiyo alipokuwa akilihutubia Bunge hili la Kumi na Moja kwenye kikao cha ufunguzi.
Je, Serikali imepanga kujenga mikoa mingapi majengo hayo ikiwemo Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan King, Mbunge wa Jang‟ombe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza kuchukua hatua za makusudi kukabiliana na uhaba wa nyumba za Jeshi la Polisi. Kwa kutumia mifuko ya Hifadhi ya Jamii, chini ya mpango wa mikopo wenye riba nafuu Serikali imeshajenga nyumba 360 katika Mikoa ya Dar es Salaam, Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia inakusudia kujenga nyumba nyingine 4,136 katika mikoa 17 ya Tanzania Bara na Zanzibar. Aidha, Serikali itaendelea kutatua changamoto za uhaba wa nyumba za askari kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, Miradi Shirikishi (PPP) na kwa kutumia fedha za bajeti ya Serikali kadri hali ya uchumi itakavyokuwa ikiimarika.
Mheshimiwa Spika, mkakati huu utakwenda sambamba na Mipango ya Maendeleo ya Serikali ukilenga kufikia idadi ya nyumba za makazi kwa askari wote waliopo sasa na watakaotarajiriwa kuajiriwa baadaye.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN) aliuliza:-
Suala la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar limekuwa likiongezeka siku hadi siku;
Je, Serikali inatambua tatizo hili na kama inatambua inachukua hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kwamba kila inapofika wakati wa Uchaguzi Mkuu hasa katika kisiwa cha Pemba baadhi ya watu hujichukulia sheria mkononi kwa kuwapiga wengine na kuharibu mali zao. Aidha, Serikali itaendelea kuongeza vikosi vya ulinzi na usalama katika maeneo yote tete na kuhakikisha utii wa sheria bila shuruti unazingatiwa. Pia Serikali itaendelea kuelimisha wananchi madhara ya kujichukulia sheria mkononi dhidi ya wengine wasio na hatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupitia Bunge lako Tukufu nitoe wito kwa wananchi wote kuacha mihemko na itikadi za kisiasa wakati na kabla ya uchaguzi kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:-
Je, Serikali haioni umuhimu wa kumaliza ujenzi wa nyumba za kambi ya Polisi Mabatini zilizoanza kujengwa tangu mwaka 2012 na sasa zinazidi kuwa magofu ili zisaidie hizo familia chache zipatazo 13?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing‟oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nyumba za kambi ya Polisi Mabatini zilianza kujengwa mwaka 2012. Kutokana na ufinyu wa bajeti nyumba hizo hazikuweza kukamilika kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetenga fedha katika mwaka wa Fedha 2016/2017 ili kukamilisha ujenzi wa nyumba hizo.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA (K.n.y MHE. MARWA R. CHACHA) aliuliza:-
Kumekuwepo na vifo vyenye utata wa kisiasa lakini inapotokea mpinzani kupoteza maisha havipewi kipaumbele katika upelelezi na hatua zinazochukuliwa:-
Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya hali hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi Tanzania inathamini maisha ya raia wake wote bila kujali rangi, kabila, itikadi za kidini na itikadi za kichama. Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo ambapo katika utekelezaji wa majukumu yake hatua mbalimbali huchukuliwa ili kuhakikisha haki inatendeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua stahiki za kisheria kwa kila aina ya mauaji yanayotokea kwa raia na endepo mazingira ya mauaji yatakuwa yanalihusu Jeshi la Polisi basi Tume huru huundwa ili kuchunguza na kutoa ushauri kwa mamlaka husika na hatua stahiki huchukuliwa dhidi ya wahusika hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutimiza wajibu wake wa kuwalinda wananchi wake pamoja na mali zao bila upendeleo wowote.
MHE. ANTONY C. KOMU (K.n.y. MHE. HAWA S. MWAIFUNGA) aliuliza:-
Kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa maadili ya utumishi ndani ya Jeshi la Polisi kutokana na hilo Askari wengi wanaonekana kukosa weledi kwa kujihusisha na matendo yanayokinzana na maadili ya utumishi wa umma:-
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha kuwa Askari wasio na sifa wanachukuliwa hatua?
(b) Je, zoezi la kuhakiki vyeti vya Askari wasio na sifa ndani ya Jeshi la Polisi limefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi lina utaratibu wa kuwachukulia hatua za kisheria askari wachache ambao wanachafua taswira na kazi nzuri inayoendelea kufanywa na Jeshi la Polisi kwa kukiuka sheria, kanuni na taratibu pamoja na kujihusisha na vitendo vinavyokinzana na maadili ya utumishi wa umma. Aidha, tumeamua kusitisha kwa muda ajira zote kwenye vyombo vyote vilivyomo ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi likiwemo Jeshi la Polisi na kupitia utaratibu wa kutoa ajira ili kuondoa uwezekano wa watu wasio na sifa kujipenyeza na kupata ajira ndani ya vyombo vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi la uhakiki wa vyeti vya askari wasio na sifa ndani ya Jeshi la Polisi linaendelea. Mpaka sasa jumla ya askari 19 wamechukuliwa hatua mbalimbali za kisheria.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-
Wilaya ya Liwale ilipandishwa hadhi kuwa Wilaya kamili tangu mwaka 1975, lakini ni Wilaya ya pekee ambayo haina Kituo cha Polisi wala nyumba za watumishi wa kada hiyo:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga jengo la kituo cha Polisi Wilaya ya Liwale sambamba na nyumba za watumishi ambao wanaishi uraiani kwa sasa?
(b) Je, ni lini Tarafa ya Kibutuka itapata kituo kidogo cha Polisi ili kulinda wafanyabiashara wa mazao ya ufuta wanaokuja Tarafani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamedi Kuchauka, Mbunge wa Liwale, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, siyo kweli kwamba Wilaya ya Liwale ndiyo Wilaya pekee nchini ambayo haina Kituo cha Polisi na nyumba za watumishi. Liwale ni miongoni mwa Wilaya 65 nchini ambazo bado hazijajengewa vituo vya Polisi.
Hata hivyo, Serikali itajitahidi kujenga vituo vya Polisi awamu kwa awamu kadri hali ya kibajeti itakavyoruhusu.
(b) Mheshimiwa Spika, ili kusogeza huduma za Polisi kwa wananchi ni azma ya Serikali kujenga Kituo cha Polisi kila Tarafa, sanjari na kupeleka Wakaguzi wa Polisi kuongoza vituo hivi, hata hivyo, Kata nne ikiwemo Kibutuka, Mirui, Kiangala na Nangano za Tarafa ya Kibutuka, kuna Askari Kata ambao wanatoa huduma kwa wananchi. Aidha, katika kutekeleza azma hii tayari Jeshi la Polisi limeshapeleka Wakaguzi katika baadhi ya Tarafa. Tunaomba Mheshimiwa Mbunge kuwa na subira kwani hali ya fedha itakaporuhusu mpango huu utafika kila Tarafa ikiwemo Kibutuka.
MHE. PASCAL Y. HAONGA (K.n.y. MHE. FRANK G. MWAKAJOKA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya Zimamoto katika Mpaka wa Tunduma ili kuokoa mali za wafanyabiashara wanaosubiri kuvuka pindi ajali ya moto inapotokea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika Halmashauri ya Mji wa Tunduma lina kituo katika eneo la Mtaa wa Kilimanjaro, Wilaya ya Momba katika Mkoa wa Songwe kinachohudumia Wilaya zote ukiwemo mpaka wa Tunduma. Kwa sasa kituo hiki kina gari moja lililopo matengenezoni Mjini Mbeya. Hata hivyo, Askari wanaendelea kutoa Elimu ya Kinga na Tahadhari ya Majanga ya Moto na Utumiaji wa Vifaa kwa Huduma za Kwanza, sambamba na ukaguzi wa majengo na kutoa ushauri kwa wakandarasi na makampuni ya ujenzi kuhusu ujenzi bora wa miundombinu yenye usalama kwa umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kupeleka huduma ya zimamoto katika maeneo yote nchini ikiwemo Tunduma. Hata hivyo azma hii nzuri inategemea sana upatikanaji wa rasilimali fedha. Serikali itaendelea kusogeza huduma za zimamoto na uokoaji katika maeneo mbalimbali nchini karibu na wananchi kadri hali ya upatikanaji fedha itakavyoruhusu.
MHE.FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-
Magari yanayobeba abiria nchini yamekuwa yakitozwa faini pindi yanapokamatwa kwa kosa la kujaza abiria zaidi ya uwezo wake badala ya kutakiwa kupunguza abiria waliozidi.
(a) Je, Serikali haioni kuwa kutoza faini na kuacha gari liendelee na safari huku likiwa limejaza ni sawa na kuhalalisha kosa?
(b) Je, Serikali haioni kuwa ikiwashusha abira waliozidi itakuwa imetoa fundisho na kupunguza ajali kwa abiria ambao hupanda gari huku wakijua limejaa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Usalama Barabani Sura ya 168, kifungu cha 58 ni kosa kwa abiria au mtu yeyote kutokuwa na kiti cha kukaa ndani ya gari la abiria na hivyo mtu huyo atahesabika kwamba amening‟inia ndani ya gari hilo. Mabasi yanatozwa faini kwa kuzidisha abiria yakiwa kituoni na maeneo salama abiria wote waliozidi huteremshwa na kurudishiwa nauli zao na utaratibu wa kuwatafutia mabasi mengine ambayo yana nafasi. Aidha, pale ambapo mabasi haya yalizidisha abiria yakikamatwa katika maeneo ambayo si salama huachwa na kuendelea na safari kisha mawasiliano hufanyika katika vituo vya polisi vilivyopo mbele ili abiria washushwe kwenye maeneo ambayo ni salama kwa abiria.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani imekuwa ikiwashusha abiria waliozidi ndani ya basi hasa pale inapokuwa imeonekana maeneo wanayoshushwa ni salama kwa maisha na mali za abiria hao na kutafutiwa usafiri mwingine.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:-
Askari wa Jeshi la Polisi na Magereza wanaishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi ukilinganisha na kazi zao wanazofanya kwa jamii.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaboreshea makazi.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yalivyowahi kujibiwa maswali kama haya ndani ya Bunge lako Tukufu mara kadhaa kuhusu Askari kuboreshewa makazi yao, Serikali inafahamu kuwa lipo tatizo la baadhi ya Askari wa Jeshi la Magereza na Polisi kuishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo hili Serikali imeendelea na mpango wa kuzifanyia ukarabati mkubwa baadhi ya nyumba kwenye baadhi ya magereza na kujenga nyumba mpya. Mahitaji ya nyumba hivi sasa ni nyumba 14,500 wakati zilizopo ni 4,221 hivyo kuwepo kwa upungufu wa takribani nyumba 10,279 ambao unalazimisha baadhi ya Askari wa Magereza kuishi nje ya kambi za jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Magereza limesaini mkataba na kampuni ya Poly Technologies ya China kwa kujenga nyumba 9,500 kwenye vituo vyote vya magereza nchini. Mgawanyo wa ujenzi wa nyumba hizo ni Makao Makuu Magereza nyumba 472, Mkoa wa Arusha nyumba 377, Dar es salaam 952, Dodoma 356, Kagera 364, Kigoma 272, Kilimanjaro 390, Lindi 233, Manyara 206, Mara 378, Mbeya 622, Iringa 336, Morogoro 669, Mtwara 215, Mwanza 398, Pwani 384, Rukwa 358, Ruvuma 320, Shinyanga 337, Singida 299, Tabora 408, Tanga 382, KMKGM Dar es Salaam 219, Chuo cha Ukonga 115, Chuo cha Kiwira 183, Chuo cha Ruanda 62, Chuo cha KPF 27, Bohari Kuu 82 na Bwawani 84.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jeshi la Polisi, Serikali inakusudia kujenga nyumba 4,136 katika Mikoa 17; hii Mikoa 17 tunayozungumzia, tafsiri yake ni kwamba Mikoa 15 ya Tanzania Bara na Mikoa mitano ya Zanzibar, wameichukulia Unguja na Pemba kama Mkoa kitu ambacho siyo sahihi. Kwa hiyo usahihi wake ni kwamba Mikoa 15 ya Tanzania Bara na Mikoa 5 ya Zanzibar inafanya kuwa Mikoa 19 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimeona nifanye marekebisho kwa sababu mara nyingi tumekuwa tukizungumza hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali itaendelea kutatua changamoto za uhaba wa nyumba kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, miradi shirikishi na kwa kutumia fedha za bajeti ya Serikali kadri hali ya uchumi itakapokuwa ikiimarika. Mkakati huu unakwenda sambamba na mipango ya maendeleo ya Serikali ikilenga kufikia idadi ya nyumba za makazi kwa askari wote waliopo sasa na watakaoajiriwa baadaye.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Kwa miaka ya hivi karibuni vifo vya Watanzania kutokana na ajali za barabarani vimekuwa vingi na kuleta hisia kwamba hali hii sasa ni janga la Kitaifa, ni muhimu Watanzania wakafahamu kwa takwimu kuhusu ukubwa wa tatizo la vifo na majeruhi kutokana na ajali za barabarani badala ya kusikia taarifa ya tukio moja moja:-
(a) Je, takwimu ni zipi na mchanganuo wa matukio kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 Kitaifa na Mikoa miwili inayoongoza na yenye ajali chache?
(b) Je, mfumo gani endelevu kama upo, wa wazi ambao Serikali inatumia kutoa takwimu hizi kwa Watanzania badala ya taarifa moja moja pindi inapotokea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013 zilitokea ajali 23,842 zilizosababisha vifo karibu 4,002 na majeruhi 20,689. Mwaka 2014 kulitokea ajali 14,260 zilizosababisha vifo 3,760 na majeruhi 14,530 na mwaka 2015 zilitokea ajali 8,337 zilizosababisha vifo 3,464 na majeruhi 9,383.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikoa ambayo imeongoza kwa ajali kwa mwaka 2013 ni Mikoa ya Kipolisi ya Kinondoni, ambao ulikuwa na ajali 6,589 na Mkoa wa Kipolisi wa Ilala ambao ulikuwa na ajali 3,464 na mkoa ambao ulikuwa na ajali chache ilikuwa ni Simiyu ambao ulikuwa na ajali 67 na Tanga ajali 96. Mwaka 2014 mikoa iliyoongoza kwa ajali ni Mikoa ya Kipolisi Kinondoni ambapo ajali zilikuwa ni 3,086 na Mkoa wa Kipolisi wa Ilala ulifuata kwa kuwa na ajali 2,516. Mikoa ambayo ilikuwa na ajali chache kwa mwaka huo ilikuwa ni Kagera ambayo ilikuwa na ajali 29 na Simiyu ajali 55. Mwaka 2015 Mkoa wa Kipolisi ya Ilala ajali 1,431 na Temeke ajali 1,420 ambayo ndiyo iliyokuwa inaongoza kwa mwaka huo. Mikoa ambayo ilikuwa na ajali chache kwa mwaka 2015 ni Mkoa wa Rukwa ambao ulikuwa na ajali 53 pamoja na Mkoa wa Arusha ambao ulikuwa na ajali 53.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo endelevu wa wazi uliopo wa kutoa takwimu za kupitia taarifa za mwaka za Jeshi la Polisi (Police Annual Reports) ambapo kila Mtanzania anaweza kupata taarifa hizo za ajali.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:-
Ni muda mrefu sasa Kikosi cha Polisi Marine Pemba hakina boti ya doria hali inayopelekea polisi kushindwa kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
(a) Je, Serikali inatambua hilo?
(b) Kama inalitambua, je, ni lini Serikali itakipatia Kikosi cha Polisi Marine Pemba boti za doria ili kuwawezesha polisi hao kufanya kazi zao kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mbunge wa Wingwi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inalitambua tatizo la Polisi Wanamaji Pemba kukosa boti ya doria. Serikali itawapatia Polisi Wanamaji Pemba boti pale uwezo wa kibajeti utakapoongezeka kwani boti zilizopo haziwezi kuhimili mkondo wa maji uliopo Nungwi kuelekea Pemba.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
(a) Je, ni lini askari wa Iringa watajengewa nyumba?
(b) Je, ni kiasi gani cha fedha wanachodai askari wa Mkoa wa Iringa posho na stahiki zao zingine?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la ukosefu wa nyumba za askari wa Jeshi la Polisi hapa nchini. Lengo la Serikali ni kujenga nyumba hizo kwa awamu kutegemea na upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kugharamia ujenzi huo. Kwa nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wa suala hili na pia amekuwa akijitoa sana katika kuboresha mazingira ya askari katika eneo lake.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua madai ya askari ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa kama ilivyo kwa Mikoa mingine hapa nchini. Askari wa Mkoa wa Iringa wanaidai Serikali jumla ya shilingi 431,147,410 na uhakiki wake unaendelea chini ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani ili Serikali iweze kulipa baada ya ukaguzi huo.
MHE. KHAMIS M. ALI aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa baadhi ya wakuu wa Vituo vya polisi hasa Zanzibar hutumia pesa ao za mishahara kulipa huduma za umeme katika vituo hivyo;
Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuwalipa au kuwarejeshea pesa wanazotumia kulipa umeme katika vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khamisi Mtumwa Ali Mbunge wa Kiwengwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikirejesha fedha hizo za umeme endapo askari amelipia au amenunua umeme kwa ajili ya kituo cha polisi kwa kupitia utaratibu wa kujaza fomu za madai na kuambatisha risiti ya malipo hayo kisha kuziwasilisha kwa mhasibu kwa ajili ya malipo yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Wizara yangu imekuwa ikijitahidi kupeleka fedha za kulipia umeme kwa wakati ili kuondoa usumbufu unaojitokeza kwa askari walioko vituoni na makambini kadri ya hali ya uwezo utakapokuwa unaruhusu.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma umekumbwa na wimbi kubwa la wakimbizi wa kutoka Burundi na Congo (DRC), kutokana na wimbi hilo ujambazi umeongezeka sana.
Je, Serikali iko tayari kuongeza ulinzi wa kutosha na vitendea kazi vya kutosha ili mamlaka husika iweze kukabiliana na tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba suala la wakimbizi kuja nchini hutokea mara nchi jirani zinapokuwa katika hali tete ya usalama katika nchi zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiongeza ulinzi pamoja na vitendea kazi ikiwemo magari na pikipiki kwa lengo la kudhibiti uhalifu unapojitokeza katika maeneo mbalimbali. Aidha, hivi karibuni Mkoa wa Kigoma umepokea magari 11 na Serikali itaendelea kuongeza na kuimarisha ulinzi katika Mkoa wa Kigoma na mahali pengine popote nchini ambapo kutakuwa na tatizo kama hilo.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-
Mgodi wa GGM – Geita unaongoza kwa kuwapiga vijana na kuwachapa viboko na pengine kuwasababishia vifo, lakini wahusika hawachukuliwi hatua stahiki.
Je, Serikali inachukua hatua gani sasa dhidi ya wahusika pale inapotokea wameua watu au kujeruhi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na vitendo vya uonevu na matukio kadhaa baina ya wamiliki wa Mgodi wa GGM na wananchi wanaozunguka mgodi huo. Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua stahiki kwa watuhumiwa mara tu taarifa zinapotolewa polisi. Mathalani, tarehe 14/2/2016 majira ya saa 07.15 ndani ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita, watu wawili walijeruhiwa kwa kupigwa risasi za mpira wakiwa wanaondolewa na mlinzi ambapo mtuhumiwa alikamatwa na kufikishwa mahakamani na kufunguliwa kesi Na. CC67/2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kwenye Bunge lako hili Tukufu kutoa rai kwa wananchi wanaozunguka mgodi wa Geita kuheshimu sheria na taratibu ili kuepuka vitendo vya kuvamia mgodi vinavyoweza kusababisha madhara kwao.
MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:-
Hali ya magereza nchini ni mbaya hivyo kufanya vigumu katika utoaji wa haki za kibinadamu licha ya kwamba nchi imekuwa ikijali sana utekelezaji wa mikataba mbalimbali ya kikanda na ya kimataifa katika utoaji wa haki hizo za wafungwa.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha hali hiyo katika magereza nchini?
(b) Je, Serikali imejenga magereza mapya mangapi katika kipindi cha miaka 20 iliyopita?
NAIBU WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mathayo Simba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kuboresha hali ya magereza nchini kwa awamu kadri ya fedha zitakavyopatikana. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga fedha katika fungu la maendeleo na matumizi mengineyo kwa ajili ya ukarabati, upanuzi, ujenzi wa mabweni mapya, majengo ya utawala na ununuzi wa vifaa mbalimbali vya malazi katika magereza nchini ili kuboresha huduma kwa mahabusu na wafungwa kukidhi vigezo vya haki za binadamu.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka 20 iliyopita Serikali imejenga magereza mapya 11 kwa mchanganuo ufuatao:-
1. Gereza la Mkuza- 1996;
2. Gereza la Mbarali - 2003;
3. Gereza la Igunga - 2003;
4. Geeza la Meatu - 2003;
5. Gereza la Mgagao - 2004;
6. Gereza la Kinegele - 2005;
7. Gereza la Mbozi - 2005;
8. Gereza la Mbinga - 2007;
9. Gereza la Chato - 2008;
10. Gereza la Kiteto - 2009; na
11. Gereza la Karatu - 2010.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo magereza hayo pamoja na ujenzi kutokamilika yanaendelea kutumika isipokuwa Gereza la Chato na Gereza la Karatu.
MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya kihalifu nchini yanayohusishwa pia na upatikanaji wa hati za kusafiria zaidi ya moja zinazotolewa hapa Tanzania kwa baadhi ya wahalifu kiholela:-
Je, Serikali inachukua hatua gani katika udhibiti wa utoaji hati za kusafiria kiholela?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji hutoa Pasipoti na Hati za Kusafiria kwa raia yeyote wa Tanzania kwa mujibu wa Sheria ya Pasipoti na Hati za Kusafiria Na. 2 ya mwaka 2002 ili mradi amekidhi matakwa ya sheria hiyo. Pasipoti na Hati za Kusafiria hazitolewi kiholela kwa wahalifu kama Mheshimiwa Mbunge alivyouliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutolewa Pasipoti au Hati ya Kusafiria, Idara ya Uhamiaji hufanya uchunguzi wa kujiridhisha kama mwombaji ni raia wa Tanzania na kama hana makosa kihalifu. Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji huchukua hatua zifuatazo ili kudhibiti utoaji holela wa Pasipoti pamoja na Hati za Kusafiria:-
(i) Kuwasiliana na idara mbalimbali ili kujiridhisha nyaraka zilizoambatishwa kwenye ombi la Pasipoti au Hati za Kusafiria mfano RITA;
(ii) Kuchukua hatua za kisheria na za kinidhamu kwa watumishi wanaobainika kujihusisha katika utoaji wa Pasipoti au Hati za Kusafiria kwa kukiuka sheria, kanuni na taratibu;
(iii) Kuweka masharti katika utoaji wa Hati za Kusafiria kwa mwombaji aliyeibiwa au kupoteza Hati za Kusafiria;
(iv) Kuwachukulia hatua za kisheria waombaji wa Pasipoti wanaotumia njia za udanganyifu;
(v) Kutuma taarifa za Pasipoti zilizopotea au kuibiwa kwenye Shirika la Polisi la Kimataifa (Interpol) ili kuwakamata wahusika;
(vi) Kuimarisha mfumo wa utunzaji wa kumbukumbu na takwimu za Watanzania walioomba na kupewa Pasipoti Makao Makuu ya Uhamiaji; na
(vii) Kuweka mfumo wa kielektroniki wa utoaji Pasipoti ili kuweza kutambua watu kwa usahihi na kuondokana na tatizo la kughushiwa kwa Pasipoti.
Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Uhamiaji pia hufuta Pasipoti za watu ambao wamepatikana na hatia za makosa ya biashara ya madawa ya kulevya, utakatishaji fedha, usafirishaji haramu wa binadamu, vitendo vya kigaidi au hata shughuli yeyote haramu kwa mujibu wa Sheria ya Pasipoti na Hati ya Kusafiria Na. 20 ya mwaka 2002.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-
Mradi wa REA II ulitarajia kuvipatia umeme vijiji vyote vya Jimbo la Busega na kumekuwepo na kusuasua kwa utekelezaji wa mradi huo jimboni humo:-
(a) Je, mpaka sasa ni vijiji vingapi vimepatiwa umeme kupitia mradi huo?
(b) Je, ni lini vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya vijiji 13 vimepatiwa umeme katika Jimbo la Busega kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya II unaoendelea kutekelezwa hivi sasa. Mradi huu utakamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016 ambapo vijiji vyote 18 vitapatiwa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme Wilaya ya Busega inayotekelezwa na Mkandarasi Sengerema Engineering Group inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 91.6; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 52; ufungaji wa transfoma 33 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 932.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi umekamilika kwa asilimia 94 ambapo ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 umekamilika kwa asilimia 97; ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 0.4 umekamilika kwa asilimia 93 na transfoma 18 zimefungwa. Wateja 420 wameunganishiwa umeme. Kazi hii itagharimu jumla ya shilingi bilioni 4.88.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji ambavyo havikujumuishwa katika mradi kabambe wa REA Awamu ya II vitapatiwa umeme katika Mradi wa REA Awamu ya III utakaoanza mwezi Julai, 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika maeneo hayo itajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 68; ujenzi wa njia ya umeme ya kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 198; na ufungaji wa transfoma 19 za ukubwa mbalimbali. Pamoja na kazi hizo pia wateja 6,096 wataunganishiwa umeme. Kazi hii itagharimu shilingi bilioni 8.6.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-
Askari Polisi wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Kimara wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu kwani kituo ni kidogo na maslahi yao yamekuwa duni:-
(a) Je, ni wapi na lini kituo kipya kitajengwa ili kuboresha huduma na usalama Jimboni Kibamba?
(b) Je, hatua gani zimechukuliwa kuboresha maslahi ya Askari hao ikiwa ni pamoja na kuwaongezea motisha?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA (K.n.y. NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kipolisi Kimara ilianzishwa kufuatia kuundwa kwa Kanda Maalum ya Polisi Dar es Salaam chini ya Mpango wa Maboresho ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2006 kwa lengo la kuboresha ufanisi na kuongeza huduma za ulinzi na usalama kwa wananchi. Kutokana na uhaba wa rasilimali fedha, huduma za polisi zilianza kutolewa katika jengo la kituo kidogo cha Polisi Mbezi Luis.
Mheshimiwa Naibu Spika, jengo hilo halikidhi hadhi ya kuwa Kituo cha Polisi Wilaya na pia lipo kwenye hifadhi ya barabara kuu ya Morogoro. Serikali itajenga kituo kipya eneo la Luguruni muda wowote kuanzia sasa. Aidha, hali ya vitendea kazi imezidi kuboreshwa ambapo hivi karibuni Wilaya ya Kimara imepatiwa gari lingine lenye namba PT 3696 Toyota Land Cruiser kuimarisha ulinzi wa eneo hilo.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha maslahi ya kuongeza motisha kwa askari wa Jeshi la Polisi, hivi karibuni Serikali imeongeza posho ya chakula, yaani Ration Allowance toka shilingi 180,000 hadi kufikia shilingi 300,000 kwa mwezi, kupandisha viwango vya mishahara sambamba na kuendelea kutoa huduma ya Bima ya Afya.
MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. ALLY SALEH ALLY) aliuliza:-
Wapo askari polisi kadhaa ambao wamestaafu kwa zaidi ya miaka 20 sasa na wametumikia nchi kwa uadilifu na uzalendo, lakini hawajalipwa stahili zao; Serikali kwa mara ya mwisho iliwasiliana nao kupitia barua CAB/336/394/01/70 ya tarehe 28 Julai, 2015:-
(a) Je, ni kwa nini Serikali haijawajibu barua yao zaidi ya miezi sita?
(b) Je, ni kwa nini suala hili halimalizwi kwa miaka yote ili wahusika wapate haki zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA (K.n.y. NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Wizari ya Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, (a) siyo kweli kwamba wastaafu hawa hawajajibiwa kwa zaidi ya miezi sita, bali kumbukumbu zinaonyesha kuwa Jeshi la Polisi limeshawaandikia barua ya kuwajibu askari hao tangu tarehe 12/10/2015 yenye kumbukumbu namba PHQ/C.10/8A/VOL.9/90.
Mheshimiwa Naibu Spika, (b) suala hili halina utata wowote kwani wastaafu hawa hawana wanachodai Jeshi la Polisi kwani haki zao walishalipwa kulingana na mikataba yao, kwani walikuwa chini ya mkataba wa bakishishi (gratuity) ambao ulikuwa ni uchaguzi wao.
MHE. MUSA R. NTIMIZI aliuliza:-
Wilaya ya Uyui ni Wilaya mpya ambayo makao yako Isikizya na Jeshi la Polisi tayari limehamia yaliko Makao Makuu ya Wilaya, lakini mazingira ya hapo kwa askari polisi ni magumu sana kwa sababu hakuna maji, hakuna nyumba za kuishi askari hao ambao kwa sasa wanaishi kwenye nyumba za kupanga au kwenye mabanda ya mabati yaliyojengwa karibu na kituo.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira hayo kwa askari wetu ili wafanye kazi katika mazingira bora zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Wizari ya Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa vituo vya polisi, majengo ya utawala na nyumba za kuishi askari ni suala ambalo linahitaji fedha nyingi kwa nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na upungufu mkubwa kwenye Vituo vya Polisi Daraja la A na B ni vituo ambavyo vinatakiwa kujengwa katika Mikoa na Wilaya za Kipolisi na Miji inayokuwa. Vituo vya Daraja A vinavyotakiwa kujengwa nchi nzima ni 94 kwa wastani wa shilingi bilioni 94, Vituo vya Daraja B vinahitajika 382 kwa gharama ya shilingi bilioni 191 na Vituo Daraja C 4,043 kwa gharama ya shilingi bilioni 950.
Mheshimiwa Naibu Spika, majengo yanayotakiwa na Makamanda ni 15 wastani wa shilingi bilioni 15, nyumba za kuishi Askari ni zaidi ya 35,000 wastani wa shilingi trilioni mbili nukta nane.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga kufanya yafuatayo, ili kukabiliana na tatizo hili la miundombinu ya Jeshi la Polisi:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, nyumba za kuishi askari Serikali ina mpango wa kujenga nyumba 3,500 kila mwaka kwa nchi nzima. Serikali kwa Awamu hii ya Tano ina mpango wa kujenga nyumba 4,136 za mkopo kutoka Serikali ya China na tayari mpango huo upo Wizara ya Fedha, mkopo utakaogharimu dola za Kimarekani zinazokisiwa kuwa milioni 500.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Vituo vya Polisi Daraja A, B na C na majengo ya makamanda, Serikali itaendelea kujenga vituo hivi kulingana na uwezo na upatikanaji wa fedha.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaendelea kuwasiliana na Serikali za Mitaa, ili pale inapoanzishwa Wilaya au Mikoa mipya kuwepo na huduma zinazohusiana na masuala ya ulinzi na usalama, ikiwa ni pamoja na kujenga vituo vya polisi na nyumba za kuishi askari.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-
Askari wa usalama barabarani ndio wenye dhamana ya kuhakikisha usalama wa watumiaji wa barabara, lakini kwa sasa askari hao wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya rushwa na ukosefu wa maadili.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha askari wa usalama barabarani wanakuwa waadilifu na hawajihusishi na vitendo vya rushwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mhehimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi limekuwa na mikakati ya kuhakikisha askari wa usalama barabarani hawapokei rushwa kwa kufanya yafuatayo:-
(i) Kutoa elimu wa askari wote wakiwemo wa usalama barabarani juu ya madhara ya rushwa katika mabaraza, kwenye komandi na vikosi, ikiwa ni pamoja na kutoa maelekezo kwa askari kabla ya kuingia kazini na baada ya askari kutoka kazini.
(ii) Kutoa namba za simu za viongozi wa polisi, viongozi wa mamlaka nyingine za ulinzi na usalama kwa umma.
(iii) Mfumo wa kutoa notification kwa kutumia mashine za kielektroniki ambayo nimoja wapo ya mkakati wa kukomesha rushwa barabarani.
(iv) Kusambaza mabango katika maeneo mbalimbali yanayopiga vita rushwa.
(v) Kuanzishwa kwa masanduku ya maoni ili kutoa malalamiko katika vituo vya polisi.
(vi) Kuwasimamia na kuwakagua mara kwa mara askari hawa katika maeneo yao ya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mikakati hiyo Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaojihusisha na vitendo vya rushwa.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA (K.n.y. MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM) aliuliza:-
Kumekuwepo na ajali nyingi zinazosababisha vifo na majeruhi barabarani, baharini na kwenye maziwa.
Je, ni ajali ngapi zimetokea barabarani, baharini na kwenye maziwa kuanzia Januari, 2015 hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Masoud Abdalla Salim, Mbunge wa Mtambile, lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Kakunda Joseph, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi cha Januari, 2015 hadi Februari, 2016 jumla ya ajali zilizotokea ni 9,864 ambazo zimesababisha vifo 3,936 na majeruhi 9,868 katika Mikoa yote ya Tanzania Bara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi kama hicho jumla ya ajali 15 za baharini na kwenye maziwa zilizotokea, ambapo tisa zilitokea baharini na sita zilitokea katika maziwa. Katika ajali hizo, jumla ya watu 24 walipoteza maisha na watano walijeruhiwa.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA (K.n.y. MHE. RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-
Kumekuwa na sintofahamu katika eneo la Kata ya Misunkumilo, Wilaya ya Mpanda Mjini, Wanajeshi wanadai eneo hilo ni la Jeshi, lakini makazi ya wananchi yalitangulia na wana hati ya maeneo yao:-
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutatua jambo hili ikiwa Jeshi limewakuta wananchi katika eneo hili?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na sababu za kistratejia, JWTZ lilipewa eneo la Misunkumilo lililopo Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda mwaka 1985 lenye ukubwa wa hekta 3195. Serikali ililipa fidia kwa wananchi waliokuwepo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1992 Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania lilihamisha kombania yake kutoka katika eneo hilo ila eneo alikabidhiwa Mkuu wa Wilaya kwa uangalizi. Kutokana na sababu za kiusalama hasa ukanda wa Ziwa Tanganyika, imebidi Jeshi lirejee kwenye sehemu hiyo tena. Hata hivyo, sehemu ya eneo hili sasa limevamiwa na kupangiwa matumizi mengine na uongozi wa Manispaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 16 Novemba, 2015 kilifanyika kikao cha pamoja kati ya JWTZ na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Katavi. Maamuzi yaliyofikiwa katika kikao hicho ni kulipima upya eneo hilo kwa kuzingatia maendeleo yaliyopo, lakini vile vile na mahitaji ya JWTZ.
Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi eneo hili litapungua kutoka ekari 3,195 za awali hadi 2,235. Zoezi la kupima upya litakuwa shirikishi na litatekelezwa mara fedha zitakapopatikana katika mwaka wa fedha wa 2016/2017.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-
Jeshi la Polisi nchini linafanya kazi kubwa na muhimu ya kulinda usalama wa raia na mali zao, lakini linakabiliwa na upungufu mkubwa wa makazi kwa Askari wake:-
(a) Je, Serikali imepanga kujenga majengo mangapi katika Wilaya Mpya ya Itimila na Busega kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuyakamilisha makazi ya Askari Polisi yaliyomo Wilaya ya Meatu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mwaka huu wa Fedha 2016/2017, Wilaya Mpya za Itilima na Busega hazikutengewa fedha za ujenzi. Hata hivyo, kwa kuwa Wilaya ya Itilima na Busega ni mpya hivyo kuwa na mahitaji makubwa. Katika mradi wa nyumba 4,136 unaotarajiwa kuanza punde taratibu za mkopo wa ujenzi wa nyumba hizi utakapokamilika kipaumbele ni kwa mikoa mipya ukiwemo Mkoa wa Simiyu wenye Wilaya za Itilima na Busega.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni nia ya Serikali kukamilisha miradi yote ya Makazi ya Askari nchi nzima ambayo ujenzi wake umesimama kutokana na
ukosefu wa fedha. Azma hii nzuri itategemea upatikanaji wa Fedha za Maendeleo katika Bajeti ya Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Wizara itaendelea na juhudi mbadala zikiwemo kuhamasisha Waheshimiwa Wabunge, wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo kuchangia na kushiriki katika kusaidia juhudi za Serikali za kupunguza tatizo kubwa la makazi ya Askari nchini pamoja na ofisi.
MHE.ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Vituo vya Polisi vya Kabwe na Kirando vimechakaa sana na hata polisi hawana nyumba za kuishi:-
Je, ni lini Serikali itajenga au kukarabati vituo hivyo na kuwajengea polisi nyumba za kuishi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Keissy, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa kukarabati, kujenga makazi na vituo vya Polisi nchi nzima ikiwemo Kabwe na Kirando kwa awamu. Kwa upande wa makazi ya Askari Polisi awamu ya kwanza ya ujenzi itajumuisa nyumba 4,136. Kwa vituo ambavyo ni chakavu Serikali itaendelea kuvifanyia ukarabati kulingana na uwezo wa fedha kadri utakavyoruhusu.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za Askari Polisi katika Wilaya mpya ya Songwe, hasa ikizingatiwa kuwa Maaskari wengi wameripoti ndani ya Wilaya hii mpya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Phillipo Augustino Mulugo, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua tatizo la makazi ya Askari Polisi katika Wilaya mpya ya Songwe na maeneo mengine nchini hususan kwenye mikoa mipya. Nia ya Serikali ni kutatua tatizo la upungufu wa makazi ya Askari Polisi kwa kujenga nyumba kwa awamu kupitia mpango wa ujenzi wa nyumba 4,136 nchi nzima. Mkoa wa Songwe ambao Wilaya ya Songwe inapatikana, ni sehemu ya mpango huo ambao utaanza kutekelezwa baada ya utaratibu wa mikopo kukamilika.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Kazi za Vikosi vya Ulinzi na Usalama ni kulinda raia, mali zao pamoja na mipaka ya nchi, lakini kuna baadhi yao wanakwenda kinyume na sheria kwa kuwapiga wananchi na kuwasababishia ulemavu au vifo:-
(a) Je, mpaka sasa Serikali imeshawachukulia hatua gani?
(b) Je, mpaka sasa ni askari wangapi wamekutwa na hatia na kufukuzwa kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi hufanya kazi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Hata hivyo, kuna askari wachache ambao wamekuwa wakikiuka maadili na mwenendo mwema wa Jeshi la Polisi kama ambavyo imeainishwa katika Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi, namba 103.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kinidhamu kwa watumishi wanaoonekana kwenda kinyume na maadili ya kazi za Jeshi la Polisi ikiwemo kuwapiga wananchi wasio na hatia. Mathalan, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi 2016 Juni, askari 200 walichukuliwa hatua za kinidhamu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya askari 152 walikutwa na hatia na kufukuzwa kazi.
MHE. TWAHIR AWESU MOHAMMED aliuliza:-
Kumekuwa na malalamiko ya baadhi ya watuhumiwa wa makosa mbalimbali kunyanyaswa na kupigwa na vyombo vya ulinzi na usalama hasa Jeshi la Polisi na kusababisha matatizo makubwa ya kiafya kwa watuhumiwa:-
Je, Serikali inasema nini juu ya Polisi wanaofanya vitendo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Twahir Awesu Mohammed, Mbunge wa Mkoani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa kunawezekana kukawa na malalamiko katika vituo vyetu vya Polisi kwa mujibu wa PGO Na.103 (1) inaelekeza kuwa japokuwa lalamiko ni dogo kiasi gani lazima Kamanda wa eneo afungue jalada na kuchunguza ukweli wa malalamiko hayo na ikibainika Askari aliyefanya kitendo hicho atachukuliwa hatua za kinidhamu dhidi yake kama vile kukatwa mshahara ama kufukuzwa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeweka mfumo madhubuti wa kushughulikia malalamiko hayo kwa Mikoa yote ya Polisi, Makao Makuu ya Polisi na kama haitoshi Wizarani kwangu kuna dawati la kushughulikia malalamiko.
Kwa nafasi hii, nitoe rai kwa wale wote ambao hawatendewi haki wafuate utaratibu huo na hatua zitachukuliwa kikamilifu. Pia, Jeshi la Polisi limeendelea kutoa elimu kupitia mfumo wa mafunzo kazini, vilevile mafunzo ya vitendo ili kuhakikisha kuwa Askari wote wanafanya kazi zao kwa weledi na usasa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi.
MHE. ALLY SALEH ALLY (K.n.y. MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED) Aliuliza:-
Suala la usalama wa raia na mali zao ni moja ya dhamana ya Jeshi la Polisi nchini; ni muda sasa Zanzibar wananchi wamekuwa wakipigwa, kunyanyaswa na kunyang‟anywa mali zao kunakofanywa na vikosi vya SMZ.
Je, nini kauli ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusiana na matukio hayo huko Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Muhammed Amour Muhammed, Mbunge wa Bumbwini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa usalama wa raia na mali zao ndiyo dhamana kuu au kazi ya msingi ya Jeshi la Polisi nchini. Taarifa hizo hadi sasa hazijapata uthibitisho sahihi kutoka kwa wale ambao wanadai kutendewa vitendo hivyo, kwani hakuna taarifa yoyote iliyoripotiwa kwenye vituo vya polisi Visiwani Zanzibar kuhusiana na uhalifu huo. Kwa mujibu wa taratibu zilizopo ni kwamba mtu yeyote ambaye anafanyiwa kitendo chochote cha uhalifu anapaswa kutoa taarifa kwenye kituo cha polisi, ili hatua za kiuchunguzi na kiupelelezi zifanyike ili kubaini wahalifu ambao wamehusika na hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi bado inasisitiza kuwa haitambui uwepo wa vitendo hivyo na inatoa wito kwa wananchi wote ambao watafanyiwa au wamefanyiwa vitendo kama hivyo, watoe taarifa kwenye vituo vya polisi au kwa viongozi wa polisi waliopo Makao Makuu Zanzibar na Dar es Salaam ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa dhidi ya vitendo hivyo kwa watuhumiwa.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE aliuliza:-
Pamoja na Jimbo la Kigamboni ni Wilaya ya Kipolisi, majengo ya Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Wilaya (OCD) na kituo chake ni chakavu sana:-
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha Wilaya hii inakuwa na ofisi nzuri za polisi?
(b) Je, hatua hizi zitaanza kutekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kigamboni ni moja kati ya Wilaya tano za Mkoa wa Dar es Salaam ambayo imeanzishwa mwaka 2006 chini ya mpango wa maboresho ya Jeshi la Polisi kwa lengo la kuboresha na kusogeza huduma za ulinzi na usalama karibu na wananchi. Kutokana na uhaba wa rasilimali fedha na majengo, huduma za kipolisi zilianza kutolewa katika jengo dogo la Kituo cha Polisi Kigamboni chenye hadhi ya Daraja la C.
(b) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi inakusudia kujenga vituo vyote vya polisi kwenye Wilaya ambazo hazina majengo yenye hadhi stahiki ikiwemo Wilaya ya Kigamboni. Ujenzi wa kituo hicho utafanyika eneo la Kibada mara fedha zitakapopatikana.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI aliuliza:-
Kumekuwa na tabia za watu kupiga watu wengine hovyo kila siku, vipigo hivyo vinafikia kiasi cha utesaji (torture) kama ilivyotokea Mbeya Sekondari kwa walimu kumshambulia mwanafunzi au mtu kumtoa macho kama ilivyotokea huko Buguruni na maeneo mengine:-
(a) Je, Serikali inaona mateso haya wanayopata Watanzania kutoka kwa Watanzania wenzao?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani ili kuwalinda wananchi na vitendo hivi vya kikatili?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hivi karibuni kumekuwepo na vitendo vya kusikitisha katika nchi yetu na kwa jamii ambavyo ni kinyume cha sheria na havikubaliki. Aidha, Serikali haikubaliani na vitendo vya namna hii vinavyofanywa na mtu/watu/ kikundi kwani vitendo hivyo ni kinyume na sheria na utaratibu mzima wa haki za binadamu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ili kuzuia na kuwalinda raia na mali zao. Aidha, Serikali kupitia Jeshi la Polisi hupokea taarifa za matukio mbalimbali na kuyafanyia uchunguzi wa kina na inapobainika upo ushahidi wa kutosha, mtuhumiwa huchukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria. Nichukue fursa hii kuwaasa sana wale wote ambao wanakiuka taratibu, kanuni na sheria za nchi waache tabia hiyo mara moja. Wizara yangu haitakuwa na suluhu na mtu yeyote atakayetenda uhalifu huo.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Jeshi la Zimamoto Mkoani Njombe linakabiliwa na ukosefu wa Ofisi pamoja na vitendea kazi hususan magari jambo linalopelekea Jeshi hilo kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi.
Je, ni lini Serikali italipatia Jeshi hilo ofisi za kudumu pamoja na magari ili liweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lina uhaba mkubwa wa ofisi na vitendea kazi katika vituo vyote nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni nia ya Serikali kuongeza bajeti kwa Jeshi la Zimamoto na uokoaji ili liweze kukabiliana na changamoto zilizopo zikiwemo uhaba wa vitendea kazi kama vile magari ya kuzimia moto, magari ya maokozi pamoja na kufanyia ukarabati ofisi zilizopo katika mikoa yote na kuliwezesha Jeshi la Zimamoto kuwa la kisasa ili kutoa huduma nzuri kwa wananchi wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nia hii njema ya Serikali itakuwa ikitekelezwa kwa mujibu wa upatikanaji mapato ya Serikali na bajeti itakayotengwa kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kila mwaka.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-
Mkoa wa Kagera umezungukwa na nchi za Rwanda, Burundi na Uganda na mipaka ya nchi hizo imekuwa adhabu kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera, kwani hali ya usalama wa raia na mali zao umekuwa mashakani kutokana na kuvamiwa na majambazi toka nje ya Tanzania wakishirikiana na baadhi ya Watanzania wasio na uzalendo na Taifa lao.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kuimarisha ulinzi katika mipaka hiyo ili wananchi wa Mkoa wa Kagera waweze kuishi kwa amani na utulivu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yako matukio ya ujambazi katika mikoa ya pembezoni ikiwemo Kagera ambapo watu toka nchi jirani wanaingia na silaha kali za kivita na kufanya unyang‟anyi wa mali za wananchi. Hii inatoka na mkoa huu kupakana na nchi ambazo zimekosa amani na kuzalisha wahamiaji haramu kuingia nchini kwetu kwa njia za panya na tukizingatia kwamba mipaka yetu imezungukwa na mapori makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama inafanya mikakati ya kutekeleza yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya operesheni za pamoja katika mipaka yetu; vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi yetu na nchi ya jirani vinafanya operasheni za pamoja na kubadilishana taarifa mbalimbali za uhalifu na wahalifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vya ulinzi na usalama hufanya misako ya kushitukiza katika mapori yote yaliyoko Kagera, Kigoma na maeneo yote ya mipakani, kwani ndiyo maficho ya uhalifu; hufanya doria na polisi kusindikiza magari katika baadhi ya maeneo tete; Kamati za Ulinzi na Usalama za maeneo husika zinafanya vikao vya ujirani mwema ili kuwaelimisha wananchi juu ya kutoa taarifa kwenye Mamlaka za Serikali husika wanapoona wageni wasiofahamika wanaingia ama kutoka katika maeneo yao.
MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-
Wilaya ya Maswa ni moja ya Wilaya kongwe hapa nchini, lakini haina kituo cha Polisi cha Wilaya:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kituo cha Polisi cha Wilaya.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayo Wilaya 162 na kati ya hizo tumefanikiwa kujenga vituo vya Polisi katika Wilaya 97. Serikali ina mpango wa kujenga vituo vya Polisi katika Wilaya 65 zilizosalia kutegemeana na upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, tumepata jengo ambalo litafanywa kuwa kituo cha Polisi cha Wilaya wakati tukisubiri utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa vituo vya Polisi nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira hadi hapo hali ya fedha itakapokuwa nzuri tutakamilisha ujenzi wa vituo vya Polisi katika Wilaya zilizosalia Maswa ikiwa miongoni mwao.
MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-

Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi katika mazingira magumu kutokana na uchakavu wa vitendea kazi pamoja na kukosekana kwa magari ya kutosha:-
(a) Je, ni lini Serikali itawapatia magari Askari Polisi wa Wilaya ya Masasi ili kupunguza ugumu wa mazingira ya kazi?
(b) Je, ni lini Serikali itarekebisha utaratibu uliopo ambapo inafikia wakati askari wanalazimika kutoa pesa zao mfukoni ili kuwapa chakula mahabusu?
(c) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za askari katika Wilaya ya Masasi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Polisi Wilaya ya Masasi kina magari mawili yanayohudumia Wilaya nzima. Hata hivyo, Serikali inatambua kuwa magari hayo hayatoshelezi mahitaji ya Wilaya. Aidha, Serikali inatarajia kupokea magari kwa ajili ya matumizi ya Jeshi la Polisi wakati wowote kuanzia sasa na mara magari hayo yatakapowasili, Wilaya ya Masasi itakuwa miongoni mwa Wilaya zitakazogawiwa magari hayo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuwahudumia mahabusu wanapokuwa mikononi mwa polisi ili kupata huduma muhimu za kijamii. Mathalani katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ilitenga zaidi ya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuhudumia mahabusu walioko vituo vya polisi, mwaka wa 2016/2017, Serikali ilitenga zaidi ya shilingi bilioni 1.7 kwa ajili ya kuhudumia mahabusu walioko Vituo vya Polisi Tanzania Bara na Zanzibar.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua tatizo la ukosefu wa nyumba za askari hapa nchini. Katika kukabiliana na tatizo hilo, Serikali ina mpango wa ujenzi wa nyumba kwa awamu kutegemea na upatikanaji wa fedha. Ndiyo maana Serikali inao mpango wa kujenga nyumba 4,136 kwa kupitia mkopo wa bei nafuu kutoka Serikali ya China kupitia Kampuni ya Polytech utakaogharimu dola za Kimarekani milioni 500.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia nyumba za makazi Askari Polisi na Magereza katika Wilaya ya Tunduru Mkoa wa Ruvuma?
(b) Je, Serikali imejipangaje kufanya ukarabati kwa nyumba za askari zilizopo Wilayani Tunduru ambazo kwa muda mrefu hazijafanyiwa ukarabati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sikudhani Chikambo, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa nyumba za makazi, maafisa na askari, Serikali imeendelea na utekelezaji wa mpango wa kujenga nyumba mpya kwenye baadhi ya magereza nchini kwa kutumia fedha zinazotengwa katika fungu la bajeti ya maendeleo kila mwaka. Kwa kutambua uhaba na uchakavu wa nyumba za Askari Polisi na Magereza, Serikali ina mpango wa kuwajengea askari nyumba 9,500 nchi nzima ikiwemo kwenye Gereza la Wilaya ya Tunduru pamoja na nyumba 4,136 kwa upande wa polisi, ikijumuisha Wilaya ya Tunduru.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo la uchakavu wa nyumba za makazi za maafisa na askari, Serikali itaendelea kuzifanyia ukarabati nyumba za Askari Magereza na Polisi nchini zikiwemo za Wilaya ya Tunduru kwa kutenga bajeti ya ukarabati kwa kila mwaka wa fedha kutegemeana na bajeti itakavyoruhusu.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI (K.n.y MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA) aliuliza:- Zanzibar kumekuwa na matukio ya uhalifu yanayojitokeza mara kwa mara. Je, Serikali ina mpango gani wa kuzuia vitendo vya uhalifu visijitokeze Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Bububu kamaifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mipango ya muda mfupi, kati na mrefu wa kukabiliana na wahalifu na uhalifu ndani ya mipaka ya nchi yetu. Mikakati iliyopo ni pamoja na:- (i) Kuwajengea uwezo wa utendaji kazi askari wote ili wawe na uwezo wa kubaini, kupeleleza na kufuatilia mitandao ya kiuhalifu hapa nchini. (ii) Kufanya misako na doria za miguu, pikipiki na magari ili kubaini na kuzuia hali zozote za kihalifu zinazoweza kujitokeza. (iii) Kuimarisha ulinzi maeneo ya mipaka yote ikiwemo ya maji ili kuzuia uhalifu. (iv) Kuimarisha kikosi cha kuzuia na kupambana na madawa ya kulevya cha polisi sambamba na madawati ya Mikoa na Wilaya kwa kushirikiana na Mamlaka ya Taifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya.
(v) Kuimarisha ushirikiano baina ya Jeshi la Polisi na taasisi nyingine nchini hasa vyombo vya ulinzi na usalama. Mheshimiwa Mwenyekiti, yakifanyika haya pamoja na mambo mengine vitendo vya uhalifu na wahalifu vitapungua nchini ikiwemo na Zanzibar.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa la mahabusu katika magereza hapa nchini kutokana na kuchelewa kwa upelelezi wa mashauri mengi.
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani za haraka ili kukabiliana na ucheleweshaji huo wa kesi zilizopo mahakamani?
(b) Je, ni muda gani umewekwa kisheria pale upande wa mashtaka unaposhindwa kupeleka ushahidi mahakamani ili mahakama iweze kumuachia huru mshitakiwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiri, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali na za haraka ili kukabiliana na ucheleweshaji wa kesi mahakamani ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa majalada ya kesi unaofanywa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) pamoja na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), kuundwa kwa Jukwaa la Haki Jinai na kutembelea mahabusu magerezani na kufanya mahojiano na mahabusu gerezani ili kushirikisha wadau wengine wa sheria katika kesi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wa kisheria wa kuondoa shauri mahakamani kama upelelezi haujakamilika ni siku 60 na mtuhumiwa kuachiwa huru.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Katika Jimbo zima la Mlimba kuna kituo kimoja tu cha polisi cha Mngeta jambo linalofanya hali ya usalama kwa wananchi kuwa duni.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya polisi katika Jimbo la Mlimba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uhaba wa vituo vya polisi nchini na ili kuimarisha usalama nchini Serikali ina mpango wa kujenga vituo vya polisi hadi ngazi ya kata na tarafa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira hadi hapo hali ya fedha itakapokuwa nzuri na kutuwezesha kutekeleza mpango huo.
MHE. SABREENA H. SUNGURA aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza ajali za barabarani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Hamza Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeandaa mkakati wa kudhibiti makosa yanayosababisha madhara makubwa ambayo hupelekea ajali za barabarani kuongezeka. Mambo yaliyolengwa katika mkakati pamoja na mambo mengine ni:-
(1) Udhibiti wa madereva walevi na kuendesha kwa uzembe;
(2) Udhibiti wa mwendokasi kwa madereva na wamiliki wa magari , kuwa na madereva wenza kwa mabasi ya safari za zaidi ya masaa manane;
(3) Kuthibiti uendeshaji magari bila sifa/leseni za udereva ama Bima;
(4) Kudhibiti usafirishaji wa abiria kutumia magari madogo yenye muundo wa tairi moja nyuma;
(5) Kusimamia matumizi ya barabara kwa Makundi Maalum mfano watoto, wazee, walemavu na wasiotumia vyombo vya moto ikiwemo mikokoteni na baiskeli;
(6) Kudhibiti ajali za pikipiki za magurudumu mawili (bodaboda) na magurudumu dumumatatu (bajaji);
(7) Kuzishauri mamlaka husika kuweka alama za kudumu za utambulisho kwenye maeneo hatarishi ya ajali;
(8) Kusimamia utaratibu wa nukta (Point System) kwenye leseni za udereva;
(9) Marekebisho ya Sheria za Usalama Barabarani;
(10) Abiria kufunga mikanda ya usalama wanapotumia vyombo vya usafiri;
(11) Kubaini maeneo tete na hatarishi ya ajali za barabarani;
(12) Kuthibiti utoaji na upokeaji rushwa barabarani;
(13) Motisha kwa askari wanaosimamia vizuri majukumu yao; na
(14) Kuwajengea uwezo wa kiutendaji askari wa usalama barabarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nidhahiri kwamba suala la usalama barabarani siyo la kundi au taasisi moja tu ila ni letu sote. Wabunge ni miongoni mwa wahusika wa suala la usalama barabarani, kwa maana kuwa nafasi yao kubwa ni katika kuelimisha umma na kusaidia katika ujenzi wa utamaduni wa kuheshimu alama za usalama barabarani nchini.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI Aliuliza:-
Moja kati ya kazi za Polisi ni ulinzi na usalama wa raia na mahali zao, uzoefu unaonesha kila zinapotokea kampeni za Uchaguzi Jeshi la Polisi hutumika kama Taasisi ya Chama Tawala hivyo husababisha ulinzi na usalama (hasa Wapinzani) kutoweka mikononi mwa Polisi:-
Je, Serikali haioni kwamba inalitumia Jeshi la Polisi kwa lengo la kudhoofisha Upinzani na kurahisisha kukipatia ushindi Chama chake cha CCM?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linafanya kazi zake kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ikiwa ni pamoja na Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi (PGO) ambazo zinatoa mwongozo kwa shughuli za Askari.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ifahamike kwamba Jeshi la Polisi lipo kwa ajili ya Ulinzi wa raia na mali zao na siyo kwa ajili ya chama fulani cha siasa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anasema. Ni Jeshi linalowatumikia Watanzania wote pasipo kujali vyama vyao, kabila zao, dini zao ama rangi zao. Hata hivyo, ikitokea Askari wamekiuka taratibu za kiutendaji tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali za kinidhamu dhidi ya wale ambao Wizara yangu inapata malalamiko rasmi kupitia dawati la malalamiko.
MHE. ESTHER N. MATIKO Aliuliza:-
Kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa leseni za udereva katika Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya kutokana na kutokuwepo kwa huduma hiyo. Hali hiyo inapelekea wananchi kupata adha kubwa ya kufuata huduma za leseni Musoma Mjini ambao ni Mkoa mwingine wa Polisi; kutokana na adha hiyo wananchi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali waliamua kujenga na kukamilisha jengo la usalama barabarani:-
(a) Je, ni lini Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya utafungiwa mitambo ya kutoa leseni za udereva ili kuondoa usumbufu uliopo sasa wa kutumia gharama na muda kufuata huduma hiyo Musoma Mjini?
(b) Je, ni lini Ofisi za Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya zitajengwa ili kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania na Jeshi la Polisi Usalama Barabarani imekuwa ikiboresha huduma za utoaji leseni za udereva na ukusanyaji wa ada za leseni ili kuhakikisha kuwa huduma hizi zinawafikia wananchi bila usumbufu. Serikali kupitia taasisi hizi imefunga mitambo ya kutoa leseni za udereva kila Makao Makuu ya Mkoa ambapo wananchi wote wanaohitaji huduma hizi hufika Mkoani na kuhudumiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufunga mitambo hii kunahitajika maandalizi makubwa ya kifedha na uandaaji wa miundombinu ya mtandao, majengo na rasilimali watu. Kwa sasa, mitambo hiyo imefikishwa hadi kwenye Mikoa ya kikodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania. Serikali ingependa kufunga mitambo ya kutoa leseni za udereva katika ngazi za Wilaya ikiwemo Wilaya ya Tarime/Rorya. Hata hivyo, kwani gharama za kufunga mitambo hii katika Wilaya zote nchini ni kubwa mno. Serikali inao mkakati wa kufikisha huduma hizi Wilayani ikiwemo Wilaya ya Tarime/Rorya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kipolisi Tarime/ Rorya ni miongoni mwa Mikoa mipya ambayo bado haijajengewa ofisi mpya za kisasa ikiwemo Songwe, Katavi, Simiyu na Geita. Serikali inatambua uhaba huo wa ofisi katika mikoa hiyo na kuna mkakati wa ndani wa kujenga ofisi hizo kwa kutumia rasilimali zilizopo kama nguvu kazi ya wafungwa na kutengeneza matofali ya kujengea ofisi hizo muhimu kwa huduma ya Kipolisi na Idara zingine za Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
MHE. ESTER A. BULAYA aliuliza:-
Kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya ujambazi na unyang’anyi wa kutumia silaha ndani ya Mji wa Bunda na wahanga wa matukio hayo ni wafanyabiashara wadogo wadogo.
Je, ni hatua zipi za kiusalama zimechukuliwa ili kukabiliana na wimbi la ujambazi na unyang’anyi katika Mji wa Bunda?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa hivi karibuni kulikuwa na wimbi la uhalifu kwa Mkoa wa Mara na mikoa mingineyo. Jeshi la Polisi limeendelea kubuni na kutekeleza mikakakati mbalimbali ya kubaini, kuzuia na kukabiliana na uhalifu, kadri uchambuzi wa uhalifu unavyoonesha mwenendo na mwelekeo wa uhalifu nchini ukitumika kama zana ya kutabiri uhalifu wa baadaye.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi limeendelea kuwajengea uwezo Maafisa Wakaguzi na Askari kwa kuyatambua na kuyaundia mikakati ya utekelezaji mambo yafuatayo:-
(i) Kutabiri mwelekeo wa uhalifu kwa kutumia takwimu za uhalifu, kumbukumbu za uhalifu pamoja na mabadiliko ya uhalifu ili kuweza kutambua maeneo korofi, wahalifu wanaohusika, mahali walipo na namna ya kukabiliana na uhalifu huo.
(ii) Kuyatambua maeneo nyeti yenye vivutio vya uhalifu na kuyapangia ulinzi pamoja na misako na doria.
(iii) Kuendelea kufanya misako na doria mara kwa mara ili kuimarisha ulinzi na usalama katika maeneo mbalimbali nchini.
(iv) Kushirikiana na wadau wote wa ulinzi na usalama kubadilishana taarifa za Kiintelijensia pamoja na uzoefu katika kuzuia uhalifu kwa kuibua mifumo mipya na kuboresha ya zamani.
Mheshimiwa Spika, kwa nafasi hii nitoe rai kwa wananchi wote kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi ili kuwabaini, kuwafichua na kuwakamata ili mkondo wa sheria uchukue nafasi yake kwani hatutasita kuchukua hatua kali dhidi ya vitendo hivi viovu nchini.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED aliuliza:-
Kwa mujibu wa Ibara ya 19(1) ya Katiba ya nchi, kila
mtu anayo haki na uhuru wa kuamini dini aitakayo, lakini pia chini ya Ibara ya 15(1) na (2) ya Katiba ni lazima sheria zifuatwe.
Je, ni kwa nini wanawake wa kiislamu wanapovaa hijabu nikabu wanavuliwa na Maafisa Usalama wanaume?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Ali Mohammed, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kweli kuwa wanawake
wa kiislaamu wanapovaa hijabu na ama nikabu wanavuliwa na maafisa wanaume wa Jeshi la Polisi. Aidha, Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazoliongoza Jeshi hilo na kwa mujibu wa PGO 103(1) ambayo inasema malalamiko yote dhidi ya Polisi lazima taarifa itolewe mara moja kwa Mkuu wa eneo na hatua za uchunguzi upelelezi ifanyike kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaombe wananchi hususani wanawake, pindi wanapofanyiwa vitendo kama hivyo, kupeleka malalamiko yao polisi au kwenye mamlaka nyingine husika ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Katika upande wa kusini mwa Jimbo la Tunduru Kusini wananchi takribani 200 wa Tanzania na Msumbiji huvuka Mto Ruvuma kila siku kutafuta mahitaji yao ya kila siku, upande wa Msumbiji wameweka Askari wa Uhamiaji ambao huwanyanyasa sana Watanzania kwa kuwapiga na kuwanyang’anya mali zao kwa kukosa hati ya kusafiria.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka Kituo cha Uhamiaji katika kijiji cha Makande Kazamoyo na Wenje ili kuwapatia Watanzania huduma ya uhamiaji?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikifanya juhudi za kuhakikisha kuwa inasogeza huduma karibu na wananchi ikiwa ni pamoja na huduma za Uhamiaji. Katika kutekeleza hilo Wilaya zilizo nyingi ikiwemo Tunduru zina Ofisi za Uhamiaji. Aidha, Serikali inatambua umbali mrefu wa takribani kilometa 90 uliopo kutoka vijiji vya Makando, Kazamoyo na Wenje kutoka Mjini Tunduru zilipo ofisi za Uhamiaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua hilo na uhitaji
wa huduma za uhamiaji katika vijiji hivyo ili kuwawezesha wanakijiji kuingia na kwenda nchini Msumbiji kihalali, tunafanya ufuatiliaji ili kujua gharama za kufungua ofisi za Uhamiaji katika kijiji cha Makando. Kwa kuanzia Ofisi hiyo itahudumia vijiji vya Kazamoyo na Wenje ili kuwawezesha kuvuka mpaka Kihalali. Tunawaomba wananchi na Mheshimiwa Mbunge kuwa na subira kwa kuzingatia kuwa suala hili linahitaji kutengewa fedha katika bajeti.
MHE. HAJI KHATIB KAI aliuliza:-
Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeimarisha kwa kuweka boti kwa ajili ya Police Marine maeneo mengi ya mito, maziwa na hata baharini ili kuzuia au kudhibiti ajali zinapotokea.
Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka huduma hiyo katika Mikoa au Wilaya ambazo hazijapata huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Haji Khatib Kai, Mbunge wa Micheweni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na mpango wa kupeleka huduma za boti kwa ajili ya Polisi Wanamaji ili kuzuia, kudhibiti ajali kwa awamu katika mikoa yote na Wilaya ambazo hazijapata huduma pale uwezo wa kibajeti utakapoimarika.
Aidha, muda huu ambapo Serikali inaendelea kutafuta fedha ili huduma hizo ziweze kupatikana, huduma hiyo ya Polisi Wanamaji itatolewa na vituo vya Wanamaji waliopo karibu kwa kufanya doria kwenye maeneo husika.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Gereza la Wilaya ya Iringa ambalo lipo jirani na Hospitali ya Mkoa wa Iringa limekuwa likisababisha usumbufu kwa wananchi wanaotembea kwa miguu hasa nyakati za usiku.
Je, Serikali ina mpango gani kwa kuondoa mwingiliano wa shughuli za kijamii na shughuli za gereza hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamindi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yalikuwepo malalamiko ya wananchi kupata usumbufu wa kuingia na kutoka Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambapo barabara ya kuingia inapita mbele ya lango la Gereza la Iringa. Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Iringa katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo, hasa baada ya kufungwa kwa barabara inayopita mbele ya gereza kuelekea hospitalini kwa watumiaji wa magari ilikutanisha uongozi wa Manispaa ya Mkoa wa Iringa na uongozi wa Jeshi la Magereza mkoani humo na kutoa maangizo yafuatayo:-
Moja, uongozi wa Manispaa ya Iringa kuandaa barabara mbadala itakayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini kwa kutumia gari; pili, uongozi wa Manispaa uandae ramani ya ukuta utakaozuia matumizi ya barabara inayopita gerezani kwa kutumia gari. Ukuta huo ulilengwa kuzuia magari kutoka eneo ambalo waenda kwa miguu wangepita bila kuingilia shughuli za gereza; na tatu, baada ya kupatikana ramani, uongozi wa gereza ulitakiwa kujenga ukuta huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza tayari limeshatekeleza maagizo hayo kwa kujenga ukuta unaotenganisha barabara ya watembea kwa miguu wanaokwenda hospitali kwa kutumia eneo la mbele ya gereza ili wasiingiliane na shughuli za gereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imeshatekeleza agizo la kujenga barabara mbadala inayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini na magari. Hata hivyo, pamoja na kujengwa kwa barabara mbadala, gereza limeendelea kuruhusu magari yanayokwenda hospitalini kutumia barabara hiyo mbele ya gereza kwa wakati wa dharura.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA aliuliza:-
Wapo wanawake ambao wamefungwa kwenye magerezani wakiwa na watoto wachanga/wadogo ambao bado wanahitaji uangalizi au huduma za mama zao.
(a) Je, Serikali imejipanga vipi katika kuwanusuru watoto hao ambao hawana hatia?
(b) Je, Serikali haioni kuwa inavunja haki za binadamu kwa kuwaweka gerezani watoto hao wasio na makosa?
(c) Je, Serikali inaweza kulipa Bunge takwimu za wanawake waliokinzana na sheria na wamefungwa kwa miaka mitano iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo mazingira ambayo watoto wadogo na watoto wachanga huingia gerezani wakiwa wameambatana na mama zao kutokana na mama zao kufungwa gerezani au kuingia mahabusu, ama mama zao kuingia wakiwa wajawazito na baadae kujifungua gerezani. Watoto hao hupokelewa na kuruhusiwa kuwepo gerezani na mama zao kwa mujibu wa Kifungu cha 144(1) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Kanuni 728 ya Kanuni za Kudumu za Jeshi la Magereza za mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuruhusu watoto kuwa na mama zao magerezani unatokana na kuzingatia maslahi ya mtoto kama inavyohimizwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki ya Mtoto (The Convention of Rights of the Child) na mikataba mbalimbali ya kikanda inayohusiana na haki za mtoto. Kwa kuwa mtoto mchanga huwa bado ananyonya, hivyo himaya stahiki ya malezi na makuzi ya awali huwa ni ya mama yake. Hata hivyo Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 imetoa nafasi kwa mtoto ambae mzazi wake wake yuko katika ukinzani wa sheria kuweza kupata malezi mbadala ambayo yanazingatia mahitaji yote ya mtoto kama ilivyo kwa mtoto yeyote yule chini ya uangalizi wa uongozi wa magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2016, idadi ya wanawake waliofungwa magerezani kutokana na kukinzana na sheria ilikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 ni 364, mwaka 2013 ni 321, mwaka 2014 ni 373, mwaka 2015 walikuwa ni 334 na mwaka 2016 ni 616. Hivyo kufanya jumla yake wote kuwa ni 2008.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi kutokana na sababu mbalimbali.
(a) Je, ni idadi ya watu wangapi waliopoteza maisha katika Jimbo la Ushetu kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015?
(b) Je, mauaji ya makundi haya yanapungua au yanaongezeka katika Jimbo la Ushetu?
(c) Je, Serikali imeshirikisha vipi jamii kupiga vita mauaji haya, vikiwemo vikundi vya dini, walinzi wa jadi (sungusungu) na uongozi wa kimila Jimboni Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2010 wazee waliouawa walikuwa wawili, mwaka 2011 wazee wanne, mwaka 2013 wazee watano, mwaka 2014 wazee waliouawa walifikia sita, mwaka 2015 walikuwa wawili, mwaka 2016 wawili na mwaka 2017 alikuwa ni mzee moja. Kwa hiyo, jumla ya wazee ambao wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwaka 2010 hadi 2017 ni wazee 22 katika Jimbo la Ushetu. Kwa upande wa walemavu wa ngozi, katika kipindi hicho hakuna mlemavu aliyeuawa wala kujeruhiwa Jimboni Ushetu ila kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka 2010 mpaka 2017 walemavu wa ngozi waliouawa walikuwa ni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mauaji ya makundi haya katika miaka ya karibuni yanapungua kutokana na misako iliyofanywa ya kuwakamata waganga wa kienyeji ambao wanapiga ramli chonganishi na kuchochea imani za kishirikina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukomesha mauaji haya, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kushirikiana na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali ndani na nje ya Jimbo hilo katika kutoa elimu ya ukatili huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikishirikiana na jamii na taasisi za kidini, vikundi vya ulinzi jamii ndani na nje ya Jimbo la Ushetu kwa kuwapa elimu wananchi ili kudhibiti maujai hayo ya kikatili.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-
Mara nyingi kumekuwa na taarifa juu ya watu wanaokamatwa na dawa za kulevya kwenye maeneo mbalimbali nchini, lakini hatuambiwi nini kinafanyika:-
Je, baada ya watu hao kukamatwa, ni nini huwa kinaendelea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa inachukua hatua mbalimbali katika kudhibiti dawa za kulevya za mashambani na viwandani. Hatua hizo zinalenga kudhibiti kilimo cha bangi, uingizaji, usafirishaji na utumiaji wa dawa za kulevya za viwandani kote nchini kwa kuwakamata watuhumiwa na kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha kuanzia Oktoba, 2015 mpaka Mei, 2017 Jeshi la Polisi limefanikiwa kuwakamata watumiaji mbalimbali ambapo watuhumiwa takribani 14,748 kesi zao zinaendelea mahakamani; watuhumiwa zaidi ya 2,000 walipatikana na hatia wakati watuhumiwa wanaozidi 600 waliachiwa huru na mahakama; na watuhumiwa wanaozidi 13,000 kesi zao ziko katika hatua mbalimbali za upelelezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu natoa wito kwa wananchi na wageni kuacha kujihusisha na biashara hii haramu kwa kuwa, hakuna atakayebaki salama kwenye mapambano haya. Serikali kupitia vyombo vyake itaendelea kuwasaka wahusika wote ili waweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
MHE. JUMA OTHMANI HIJA aliuliza:-
Kumekuwa na matukio yasiyo ya kawaida na kukaribia kuhatarisha amani katika Kisiwa cha Tumbatu:-
Je, Serikali haioni ipo haja ya kujenga Kituo cha Polisi katika Kisiwa hicho ili kukabiliana na matukio ya kiuhalifu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO NA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yako matukio ya kihalifu yanayoripotiwa kutoka katika Kisiwa cha Tumbatu na Jeshi la Polisi linafanya jitihada ya kukabiliana na wahalifu kwa kutoa huduma za ulinzi na usalama katika kisiwa hicho kwa kufanya doria kila siku. Pamoja na doria, kumeanzishwa utaratibu wa detach ambapo askari wanakwenda kulinda kisiwa hicho na kubadilishana kwa zamu ili kuimarisha ulinzi. Aidha, ipo boti yenye uwezo wa kubeba Askari kumi. Iwapo uwezo wa kifedha ukiongezeka tutajitahidi kupata boti kubwa ya mwendo kasi na yenye uwezo wa kubeba Askari zaidi ya kumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona haja ya kuwepo Kituo cha Polisi katika Kisiwa cha Tumbatu ili kusogeza huduma za ulinzi na usalama kwa kuzingatia jiografia ya kisiwa hicho na matukio ya uhalifu. Katika kutekeleza hilo, tayari Serikali imepata kiwanja chenye ukubwa wa mita za mraba 600 na makisio ya ujenzi wa kituo hicho umekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu naomba kutumia fursa hii kuhamasisha wadau na wananchi akiwemo Mheshimiwa Mbunge kushirikiana kuanza ujenzi wa kituo hiki wakati Serikali inakamilisha mipango yake ya kupata fedha.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Polisi wamekuwa wakifanya msako na kamatakamata ya waganga wa kienyeji sehemu nyingi hapa nchini:-
(a) Je, ni waganga wangapi wa kienyeji walikamtwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu?
(b) Je, ni waganga wa kienyeji wangapi walifikishwa Mahakamani na kutiwa hatiani katika kipindi hicho katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, waganga wa kienyeji waliokamatwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu ni 26 na kushtakiwa kwa makosa ya kufanya biashara ya uganga bila kibali na kupatikana na nyara za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 jumla ya waganga 16 walikamatwa na kufikishwa Mahakamani. Kati ya hao, waganga saba walipatikana na hatia kwa kufungwa miaka miwili kila mmoja au kulipa faini ambapo jumla ya watuhumiwa sita katika kesi tofauti walilipa faini ya jumla ya Sh.1,250,000/=. Mtuhumiwa wa kesi moja alihukumiwa miaka miwili bila yeye kuwepo Mahakamani, juhudi za kumsaka zinaendelea.
MHE. KANALI (MST) MASOUD ALI KHAMIS aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa Serikali imekuwa ikitoa ahadi za kutatua tatizo la usafiri kwa Jeshi la Polisi bila mafanikio. Kwa mfano, Kituo cha Polisi Mfenesini, Zanzibar hakina gari la uhakika kwa takribani miaka 10 sasa:-
(a) Je, ni lini Serikali itapeleka gari Kituo cha Polisi Mfenesini?
(b) Je, ni lini magari ambayo yamekuwa yakizungumzwa kwa muda mrefu yatawasili nchini ili kuondoa adha ya usafiri?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kanali (Mst) Masoud Ali Khamis, Mbunge wa Mfenesini, lenye sehemu
(a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Mfenesini kipo Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Wilaya ya Kipolisi Mjini Magharibi A. Mkoa wa Kaskazini Unguja una jumla ya magari 13 ambayo yanatoa huduma za doria na kazi nyingine za Polisi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mjini Magharibi ikiwemo Kituo cha Polisi Mfenesini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha Polisi Mfenesini kitapatiwa gari mara baada ya taratibu za upatikanaji wa magari utakapokamilika. Hata hivyo, gari la Mkuu wa Polisi wa Wilaya hutoa huduma pale inapotokea dharura ikiwa ni pamoja na kuwachukua mahabusu waliopo katika kituo hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, magari haya yamekuwa yakiwasili nchini awamu nchini awamu kwa awamu ambapo hadi sasa jumla ya magari 231 yamekwishawasili kati ya magari 777 yaliyokuwa yameagizwa.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Kumekuwa na uuzwaji wa silaha kiholela kama vile mapanga na visu katika barabara zetu ikiwemo Ubungo kwenye mataa hali ambayo inaleta hofu kwa raia wema.
Je, Serikali inalichukuliaje suala hilo ambalo ni hatari sana kwa usalama wa raia?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na uuzaji holela wa silaha za jadi katika maeneo mbalimbali ya barabara zetu ikiwemo katika makutano ya barabara ya Mandela na Morogoro eneo la Ubungo, Jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inatambua uwepo wa tatizo hilo na tayari hatua mbalimbali za kudhibiti hali hiyo zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya operesheni za mara kwa mara na kukamata wauzaji wa silaha za jadi barabarani kama vile mapanga, mikuki, upinde na mishale. Aidha, elimu inaendelea kutolewa kwa wafanyabiashara wa bidhaa za silaha hizo kutowapatia wauzaji wasio na eneo maalum la kufanyia biashara hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na mamlaka nyingine za Serikali linaandaa utaratibu maalum wa uuzaji wa bidhaa za aina hii na kutoa elimu kwa umma kuhusu madhara ya biashara hii na kuwashauri wananchi waipige vita na kuepuka kujihusisha nayo.
MHE. MHANDISI ATASHASTA J. NDITIYE aliuliza:-
Gereza la Wilaya ya Kibondo – Nyamisati limekuwa na ongezeko kubwa sana la wafungwa na mahabusu kwa sababu ya uwepo wa wakimbizi.
Je, Serikali haioni sasa ni wakati unaofaa kupeleka mradi mkubwa wa maji kwenye gereza hilo ili kulinda afya za raia na askari walioko kwenye gereza hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Atashasta Nditiye, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa kuna tatizo la upatikanaji wa maji katika Gereza la Kibondo. Mwaka 2010, Serikali kupitia Jeshi la Magereza lilitenga fedha kiasi cha shilingi milioni 20 kwa ajili ya kuchimba kisima kirefu na kazi hiyo ilifanywa na Wakala wa Uchimbaji Mabwawa na Visima iliyopo Ubungo Dar es Salaam. Uchimbaji wa kisima hicho ulikamilika tarehe 2 Oktoba 2010 na kilikuwa na uwezo wa kutoa lita 2,300 kwa saa ambayo ni sawa na lita 55,200 kwa siku. Kiasi hiki ni kidogo ukilinganisha na mahitaji halisi ya maji ya Gereza la Kibondo ambayo ni lita 94,870 kwa siku, hivyo kuwa na upungufu wa takriban lita 39,670 kwa siku.
Mheshimiwa Spika, mwaka 2014 upembuzi yakinifu ulifanywa na wataalam wa Jeshi la Magereza kwa kushirikiana na Mhandisi wa Mamlaka ya Maji Wilaya ya Kibondo na kushauri kuwa ili gereza hilo liondokane na tatizo la maji, Jeshi la Magereza linapaswa kuvuta maji kutoka mtandao wa maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo hadi gerezani ambapo gharama zake ilikadiriwa kuwa ni shilingi 330,492,450. Hata hivyo, kutokana na ufinyu wa bajeti, mradi huo haujatekelezwa hadi sasa. Serikali inaendelea kufanya jitihada mbalimbali ili kuhakikisha tatizo la maji Gereza la Kibondo linapata ufumbuzi wa kudumu.
MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y MHE. KABWE Z. R. ZITTO) aliuliza:-
Nchi ya DRC inaitegemea Kigoma kiuchumi kwa kiwango kikubwa hususan katika soko la bidhaa na huduma ya bandari ya Kigoma na hivyo wananchi wengi wa Kigoma kutembelea Congo na wale wa Congo kutembelea Kigoma. Changamoto kubwa ni gharama za biashara kutokana na viza kati ya nchi hizo mbili licha ya kwamba nchi hizo zote ni wanachama wa SADC na nchi za SADC hazina viza kwa raia wake.
Je, ni kwa nini Serikali ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo haziondoi viza kwa raia wake ili kudumisha biashara kati ya wananchi wake kwa lengo la kukuza Kigoma kuwa Kituo cha Biashara cha Maziwa Makuu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge napenda kumfahamisha kuwa suala la kutotozana viza ni la kimakubaliano baina ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na si kwamba nchi za SADC hazina viza kwa raia wanaotaka katika nchi moja kwenda nchi nyingine.
Mheshimiwa Spika, katika nchi za SADC ilikubaliwa kuwa kila nchi wanachama ziwekeane utaratibu na namna bora ya kuondoa hitaji la viza kwa raia wao. Kwa sasa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wenye pasipoti za kidiplomasia na utumishi hawahitaji kulipia viza kuingia Tanzania.
Mheshimiwa Spika, Tanzania na DRC zimekuwa katika mazungumzo ya muda mrefu kuhusu namna bora ya kuondoa malipo ya viza kwa raia wake wenye pasipoti za kawaida, lakini mazungumzo hayo yamechelewa kukamilika kutoka na migogoro ya ndani iliyoko katika nchi ya DRC. Hata hivyo, ni mategemeo kuwa kupatikana kwa suluhisho la kudumu la migogoro iliyoko ndani ya nchi ya DRC kutawezesha kukamilishwa kwa taratibu za kuondoa hitaji la viza baina ya hizo nchi hizi mbili kwa haraka.
KITETO Z. KOSHUMA (K.n.y. MHE. LAMECK O. AIRO) aliuliza:-
Wavuvi wa Wilaya ya Rorya wanaovua katika Ziwa Victoria wamekuwa wakitekwa, kunyang’anywa nyavu zao pamoja na injini za boti. Aidha, majambazi wanaofanya vitendo hivyo hutumia silaha nzito na inasemekana ni wanajeshi kutoka Uganda.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongea na Serikali ya Uganda ili kukomesha uvamizi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lameck Okambo Airo, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwepo na matukio ya uporaji wa nyavu na injini za wavuvi katika Ziwa Victoria. Uporaji huu unafanywa na wahalifu ambao bado Jeshi la Polisi halina ushahidi kuwa wanatoka ndani au nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na matukio ya uhalifu ikiwemo uporaji wa nyavu na injini za wavuvi katika Ziwa Victoria, Serikali kupitia Jeshi la Polisi ina mikakati ya kununua boti zenye uwezo na zenye mwendo kasi mkubwa. Boti hizi zitasaidia askari polisi kufanya doria za mara kwa mara na kufika kwenye matukio haraka. Aidha, Serikali inashirikiana na nchi jirani katika udhibiti wa pamoja kwa matukio ya uhalifu wa majini.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Jeshi la Polisi lina kazi kubwa ya kulinda usalama wa raia na mali zao, lakini cha kusikitisha ni kwamba askari wanaishi kwenye nyumba duni sana jambo ambalo linashusha hata hadhi zao hasa kwa upande wa Tanzania Zanzibar.
(i) Je, ni lini askari wetu watatengenezewa nyumba bora nao wajisikie kuwa Serikali yao inawajali?
(ii) Katika Makao Makuu ya Polisi pale Ziwani kuna majengo yaliyoachwa na wakoloni, je, kwa nini yasifanyiwe ukarabati mkubwa ili yaweze kutumiwa na askari wetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Jeshi la Polisi linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo upungufu wa nyumba za kuishi askari. Katika kukabiliana na tatizo hilo, Serikali ina mpango wa kujenga nyumba 350 za kuishi Askari Polisi Zanzibar. Katika idadi hiyo, nyumba 150 zitajengwa Pemba na nyumba 200 zitajengwa Unguja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kujenga nyumba mpya na siyo kukarabati nyumba za zamani zilizoachwa na wakoloni. (Makofi)
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-
Tarehe 25/5/2017 Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi akijibu swali Na. 274 kuhusu madai ya mkandarasi aliyejenga vituo vya polisi Mkokotoni Unguja na Madungu alisema, deni tayari limeshahakikiwa na kwamba atalipwa mara fedha zitakapotolewa lakini huu ni mwaka wa tano deni hilo halijalipwa:-
(a) Je, Serikali ina nia thabiti ya kumlipa mkandarasi?
(b) Je, Serikali inasubiri ipelekwe Mahakamani ndipo ilipe deni hilo?
(c) Je, huu ndiyo utawala bora ambao nchi yetu ina dhamira ya kuujenga?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi, lenye sehemu (a), (b), na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua madeni ya wakandarasi wote akiwemo Albatna Building Contractor na ina nia ya dhati ya kuyalipa madeni yote ya wakandarasi na Washauri Elekezi waliohusika katika miradi mbalimbali ikiwemo miradi iliyohusisha Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Jeshi la Polisi limetenga jumla ya shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya kupunguza madeni ya wakandarasi waliotekeleza miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa ujenzi wa Kituo cha Polisi Mkokotoni ambao umetengewa jumla ya shilingi milioni 200 ikiwa ni sehemu ya deni ambalo anadai mkandarasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kuwa hakuna deni la mzabuni au mtumishi ambalo halitalipwa kwani madeni yote yaliyohakikiwa yanaendelea kulipwa kwa kadri fedha zitakavyokuwa zinapatikana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Jimbo la Same Mashariki lina Kata 14 lakini lina Kituo kimoja cha Polisi kilichopo Kata ya Maore na vituo vidogo vilivyopo Kata ya Ndungu na Kihurio; vituo vyote hivyo vipo katika tarafa moja yenye kata tano, kata nyingine tisa ambazo zipo katika tarafa mbili zilizoko mlimani na zipo mbali sana na vituo hivyo vya Polisi zinapata shida sana kutoa ripoti za uhalifu. Kwa kuwa wananchi wa tarafa hizo mbili za mlimani tayari wametenga maeneo ya kuweka vituo vya Polisi:-
(a) Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Vituo vya Polisi katika Tarafa ya Mamba/Vunta na Tarafa ya Gonja?
(b) Kama Serikali ipo tayari kuanzisha Vituo hivyo vya Polisi, je, ni lini Polisi hao wataanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, najibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Vituo vya Polisi katika ngazi ya Kata na Tarafa nchi nzima, Mamba/Vunta na Gonja zikiwemo. Katika Tarafa ya Gonja kuna Kituo cha Polisi, Daraja B kinachotoa huduma za kipolisi katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tarafa ya Mamba wananchi wamejitolea eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi ambapo kwa sasa majadiliano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi kuhusu ujenzi wa Kituo cha Polisi, Daraja la B yanaendelea. Hata hivyo, kwa sasa Tarafa ya Mamba ina Kituo kidogo Daraja la C ambacho kinatoa huduma kwa wananchi katika Tarafa hiyo. Aidha, Jeshi la Polisi hufanya doria mara kwa mara katika maeneo hayo ya milimani ambayo hafikiwi kirahisi na vyombo vya usafiri kutokana na jiografia yake.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-
Tatizo la kupotea kwa watoto katika Jiji la Dar es Salaam limekuwa kubwa. Aidha, taarifa za kupotea kwa watoto hao zimekuwa zikitolewa kwenye vyombo vya habari:-
(a) Je, ni sababu zipi zinazochangia kuongezeka kwa tatizo hilo siku hadi siku?
(b) Je, kwa nini taarifa za upatikanaji wa watoto hao hazitolewi kwenye vyombo vya habari?
(c) Je, Serikali ina mkakati gani kuondoa tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri ya Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na wimbi la upoteaji wa watoto katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Jiji la Dar es Salaam. Aidha, sababu za upotevu wa watoto hawa ni pamoja na uangalifu hafifu wa watoto kutoka kwa wazazi au walezi na jamii kwa ujumla, mazingira magumu wanayoishi baadhi ya watoto, imani za kishirikina, visasi kati ya familia na kupotea kwa bahati mbaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hali hiyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kudhibiti matukio hayo kwa kutoa elimu kupitia programu ya Polisi Jamii kwa watoto mashuleni na wazazi kupitia mihadhara ya kijamii na vyombo vya habari. Jitihada hizo zimekuwa zikizaa matunda kwa kuongeza elimu ya usalama wetu kwanza miongoni mwa jamii na hivyo kuongeza umakini wa kulinda watoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha kuanzia Januari hadi Disemba, 2017 kwa Mkoa wa Dar es Salaam walipotea watoto 184, ambapo watoto waliopatikana ni 176 na watoto ambao wanaendelea kutafutwa ni nane. Jeshi la Polisi linaendelea kutoa rai kwa taasisi na idara mbalimbali kama Ustawi wa Jamii kushirikiana na kuwa na programu za pamoja ili kutoa elimu ya kumlinda mtoto wa Tanzania.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Majengo ya Kituo Afya cha Kambi ya Jeshi Migombani Unguja ni chakavu na pia ni siku nyingi sana.
Je, ni lini Serikali itajenga kituo hicho ili kiwe cha kisasa na kiendane na wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANO YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi wa Jeshi la Kujenga Taifa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Jeshi cha Migombani Zanzibar ni moja ya vituo vya tiba ambavyo huanzishwa katika kila Kikosi cha JWTZ ili kutoa huduma ya mwanzo ya tiba kwa Wanajeshi na familia zao, watumishi wa umma ikiwa ni pamoja na wananchi wanaishi jirani kabla ya kupelekwa katika hospitali za rufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni, kweli majengo ya kituo hicho na vituo vingine vya JWTZ yamechakaa na kwa sababu ni ya muda mrefu. Kutokana na uchakavu huo wa Kituo cha Kambi ya Migombani na sehemu nyingine, ni matazamio ya Wizara kuvi karabati upya vituo vyote katika mwaka wa fedha 2018/2019 kadri hali ya upatikanaji wa fedha itakavyoruhusu.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Hali ya nyumba za Polisi na Magereza nchini ni mbovu sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za askari hao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli hali ya makazi kwa Askari wetu siyo nzuri, hata hivyo Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo na kwa kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo husika kujenga makazi mapya na kufanya ukarabati wa majengo yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 12.3 fedha za maendeleo kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa makazi ya askari wetu katika maeneo mbalimbali nchini.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO aliuliza:-
Wananchi wa Jimbo la Songwe kwa michango yao wenyewe wamejenga jengo kubwa kwa ajili ya Kituo cha Polisi katika Kata ya Mpona tangu mwaka 2014 ili kupambana na majambazi wanaovamia wananchi hasa wakati wa mavuno ya zao la ufuta.
Je, ni lini Serikali itasaidia kuamlizia jengo hilo na kupeleka askari polisi ili kituo hicho kianze kutoa huduma?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Phillipo Augustino Mulugo kwa uhakika, Mbunge wa Songwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe ni kati ya mikoa mipya iliyoanzishwa hivi karibuni ambayo ina changamoto nyingi ya vituo vya polisi, ofisi pamoja na nyumba za askari kama ilivyo katika maeneo mengine ya nchini. Aidha, katika mkoa mpya wa Songwe hakuna Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa na Wakuu wa Polisi wa Wilaya mbili mpya za Momba na Songwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa jitihada alizofanya yeye na kushirikiana na wananchi wa Kata ya Mpona za kujenga Kituo cha Polisi katika eneo hilo. Aidha, kwa sasa kipaumbele ni ujenzi wa Ofisi ya Kamanda wa Mkoa pamoja na Wilaya mpya. Hata hivyo Serikali inafanya jitihada ili kukamilisha kituo hicho kulingana na upatikanaji rasilimali.
MHE. JOSEPH R. SELASINI aliuliza:-
Wananchi wa Kata za Mahinda, Ngoyoni, Mengwe na Kirongo – Samanga walifanya uamuzi wa kujenga vituo vya polisi kwa nguvu zao na vituo hivyo vimefikia hatua mbalimbali za ujenzi, lakini kutokana na kuwepo na shughuli nyingine zinazohitaji michango ya wananchi kama vile ujenzi wa vituo vya afya, zahanati na maabara wameshindwa kumalizia vituo hivyo.
Je, Serikali iko tayari kuchukua hatua za kumalizia ujenzi wa vituo hivyo njia ya kuwatia moyo wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, Mbunge wa Rombo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kupongeza sana juhudi za wananchi wa Mahida, Ngoyoni, Mengwe na Korongo kwa uamuzi wao wa kujenga vituo vya polisi kwa nguvu zao wenyewe. Kutokana na ujenzi wa vituo hivyo kuwa katika hatua mbalimbali. Serikali kupitia jeshi la polisi itafanya ukaguzi wa vituo hivyo ili kupata tathmini ya gharama zitakazohitajika katika kukamilisha ujenzi huo. (Makofi)
MHE. HAMAD SALIM MAALIM aliuliza:-
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 16 inatoa uhuru wa faragha kwa raia.
Je, kwa nini Jeshi la Polisi linapokwenda kupekua kwenye nyumba yenye mume na mke hutumia askari wa kiume peke yao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Salim Maalim, Mbunge wa Kojani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la upekuzi ni jukumu ambalo sheria imelipa Jeshi la Polisi na utaratibu wake umeainishwa wazi namna ambavyo upekuzi utafanyika kwenye maeneo mbalimbali. Kifungu cha 38 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai Sura ya 20 inatoa masharti na utaratibu wa kuweza kufanya upekuzi kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo nyumba, majengo na vyombo vya usafiri kama magari, boti na kadhalika endapo Afisa wa Polisi atakuwa amehisi na amejiridhisha pasipo na shaka kwamba kuna sababu ya kutosheleza kuwa kuna uwezekano wa kosa kutendeka au ushahidi kupatikana kuthibitisha kosa lililotendeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, upekuzi wa makazi ya nyumba yenye mke na mume sheria haijaweka masharti ya ni askari wa jinsia gani anatakiwa kufanya upekuzi. Hata hiyo, Jeshi la Polisi kwa kutumia Kanuni ya Kudumu za Jeshi la Polisi (PGO) pia kwa kuzingatia busara na utu wa mwanadamu huwa inazingatia utaratibu wa kupeleka askari wa kike na wa kiume pale upekuzi unapofanyika kwenye makazi ya mume na mke.
MHE. AIDA J. KHENAN (k.n.y MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA) aliuliza
(a) Je, kuna sheria yoyote ya nchi inayomruhusu askari polisi kumkatamata mtuhumiwa, kumpiga na kumtesa kabla hajajua kosa lake na kabla ya kufikishwa katika Kituo cha Polisi?
(b) Je, Serikali inachukua hatua zipi za kuhakikisha kuwa askari wanaofanya vitendo kama hivyo wanawajibishwa kwa mujibu wa sheria za nchi?
(c) Je, mpaka sasa ni askari wangapi wameshachukuliwa hatua za kisheria kutokana na makosa ya kujichukulia hatua mkononi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum lenye shemu (a),(b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai Sura ya 20 kifungu cha 11 kinaeleza namna ya ukamataji. Aidha, kifungu hiki mahsusi cha ukamataji hakimruhusu askari kumpiga na kumtesa raia wakati wowote anapokuwa kizuizini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Utendaji wa Jeshi la Polisi (PGO) askari yoyote anapobainika kufanya vitendo vya kupiga au kutesa raia huchukuliwa hatua za kinidhamu ikiwemo kufukuzwa kazi na au hata kufikishwa mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha januari mpaka Desemba, 2017 jumla ya askari 105 waliotenda makosa mbalimbali walichukuliwa hatua za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.
MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) aliuliza:-
Je, nini mipango ya Serikali ya kumaliza tatizo kubwa la nyumba za askari hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassoro Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna tatizo kubwa sana la nyumba za Askari za kuishi. Kwa kufahamu hilo Serikali imekuwa ikitenga bajeti ya ujenzi wa makazi ya Askari kwa awamu kulingana na uwezo uliopo. Aidha pamoja na kutenga fedha hizo Wizara yangu itajielekeza zaidi kutumia rasilimali zilizopo na teknolojia rahisi ya ujenzi wa nyumba ili kupunguza tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia ubia baina ya Serikali na sekta binafsi Jeshi la Polisi limefanikiwa kujenga nyumba 353 Kunduchi na Mikocheni, Dar es Salaam kwa ajili ya askari wa kawaida na maafisa. Aidha, Jeshi la Magereza linaendelea na ujenzi wa nyumba 320 Ukonga, Dar es Salaam kwa fedha za Serikali na lipo katika mazungumzo ya ubia na Shirika la Nyumba la Taifa utakaowawezesha kujenga nyumba 100 Msalato, Dodoma. Kadhalika, Idara ya Uhamiaji inafanya makubaliano na Shirika la Nyumba la Taifa kwa ajili ya ununuzi wa nyumba 103 Dodoma, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la kuhamia Dodoma. Utaratibu huu utaendelezwa katika Mikoa mingine ili kupunguza changamoto hii kwa Askari wetu. (Makofi)
MHE. SUBIRA K. MGALU (K.n.y. MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA) aliuliza:-
Baadhi ya vituo vya Polisi na Magereza nchini vina majengo chakavu sana vikiwemo Kituo cha Polisi Bagamoyo na Gereza la Kigongoni Bagamoyo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kujenga nyumba za Polisi na Askari Magereza Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli baadhi ya Vituo vya Polisi na Magereza nchini vina majengo chakavu ambayo yalijengwa miaka mingi iliyopita na kituo cha Polisi na Magereza Bagamoyo kikiwa miongoni mwao.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga Kituo cha Polisi, Gereza na nyumba za kuishi za Askari katika Wilaya ya Bagamoyo na Wilaya nyingine nchini zisizo na majengo hayo, ujenzi huo utajengwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha za bajeti. Sambamba na hilo, Wizara imeweka msisitizo katika matumizi ya rasilimali zilizopo kama vile ardhi ili kupunguza tatizo hili kwa kujenga vituo vya Polisi katika Wilaya 25 na Magereza katika Wialaya 52 kote nchini.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-
Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mheshimiwa Charles Kitwanga alikaririwa na vyombo vya habari mwezi Desemba, 2015, akiliagiza Jeshi la Polisi kumkabidhi majina ya watu wanaojihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya, ambazo ongezeko lake nchini lina athari hasi dhidi ya vijana ambao ni nguvu kazi ya Taifa:-
(a) Je, ni hatua gani zimechukuliwa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani katika kuwabaini, kuwachunguza na hatimaye kuwafikisha Mahakamani wale wote waliobainika kujihusisha na mtandao wa biashara za dawa za kulevya?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia vijana wanaojiingiza kwenye dimbwi la matumizi ya dawa za kulevya kuondokana na utegemezi wa dawa za kulevya nchini?
(c) Je, ni vijana wangapi kwa nchi nzima ambao kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita wamepatiwa tiba kusaidiwa kuondokana na utegemezi wa dawa za kulevya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athumani Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha kuwa kati ya Oktoba, 2015 hadi Aprili, 2017 Jeshi la Polisi lilifanikiwa kukamata jumla ya watuhumiwa 9,140 wa dawa za kulevya ambapo watuhumiwa 14,410 kesi zao zinaendelea Mahakamani na zipo katika hatua mbalimbali. Watuhumiwa 2,401 walikutwa na hatia, watuhumiwa 615 waliachiwa huru na watuhumiwa wengine 13,071 kesi zao ziko chini ya upelelezi.
(b) Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi kupitia Programu ya kuzuia uhalifu limeendelea kutoa huduma ya urekebishaji kwa waaathirika wa dawa za kulevya. Kwa kutumia vikundi mbalimbali vya michezo chini ya miradi ya kuzuia uhalifu kama vile familia yangu haina mhalifu na klabu ya usalama wetu kwanza.
(c) Mheshimiwa Spika, vijana 3,000 walipatiwa tiba katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kwa kushirikiana na wadau.
MHE: RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Tanzania imeridhia na kuingia mikataba mbalimbali ya kimataifa ikiwemo diplomasia na mahusiano.
Je, ni nchi ngapi na zipi ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea moja kwa moja kwa utaratibu wa visa on entry wakati wa kuingia ukiondoa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa maelezo kwa kuwa visa ni ruhusa inayoambatana na masharti ambayo hutolewa na nchi husika ili kuwaruhusu raia wa kigeni kuingia, kuondoka au kuwepo nchini katika muda maalum. Ruhusa hiyo inapotolewa katika vituo vya kuingilia nchini inajulikana kama visa on arrival.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa utoaji visa on arrival uko katika sura ya makubaliano ama mikataba baina ya nchi na nchi au taratibu zinazotokana na matengamano na ushirikiano wa kimataifa na kikanda. Utaratibu huu unaweza kubadilika kulingana na mahusianao na hali ya usalama kati ya nchi na nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo nchi 16 ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea katika utaratibu wa visa on arrival. Nchi hizo ni Benin, Burkina Faso, Cape Verde, Cote d’voire, Djibout, Gabon, Gambia, Ghana, Guinea, Guinea – Bessau, Liberia, Mali, Mauritania, Niger, Sierra Leone huu wa visa on arrival, pia zipo nchi 67 duniani ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea bila hitajio la visa.
MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA aliuliza:-
Wapo wanawake ambao wamefungwa kwenye magerezani wakiwa na watoto wachanga/wadogo ambao bado wanahitaji uangalizi au huduma za mama zao.
(a) Je, Serikali imejipanga vipi katika kuwanusuru watoto hao ambao hawana hatia?
(b) Je, Serikali haioni kuwa inavunja haki za binadamu kwa kuwaweka gerezani watoto hao wasio na makosa?
(c) Je, Serikali inaweza kulipa Bunge takwimu za wanawake waliokinzana na sheria na wamefungwa kwa miaka mitano iliyopita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo mazingira ambayo watoto wadogo na watoto wachanga huingia gerezani wakiwa wameambatana na mama zao kutokana na mama zao kufungwa gerezani au kuingia mahabusu, ama mama zao kuingia wakiwa wajawazito na baadae kujifungua gerezani. Watoto hao hupokelewa na kuruhusiwa kuwepo gerezani na mama zao kwa mujibu wa Kifungu cha 144(1) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Kanuni 728 ya Kanuni za Kudumu za Jeshi la Magereza za mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuruhusu watoto kuwa na mama zao magerezani unatokana na kuzingatia maslahi ya mtoto kama inavyohimizwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki ya Mtoto (The Convention of Rights of the Child) na mikataba mbalimbali ya kikanda inayohusiana na haki za mtoto. Kwa kuwa mtoto mchanga huwa bado ananyonya, hivyo himaya stahiki ya malezi na makuzi ya awali huwa ni ya mama yake. Hata hivyo Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 imetoa nafasi kwa mtoto ambae mzazi wake wake yuko katika ukinzani wa sheria kuweza kupata malezi mbadala ambayo yanazingatia mahitaji yote ya mtoto kama ilivyo kwa mtoto yeyote yule chini ya uangalizi wa uongozi wa magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2016, idadi ya wanawake waliofungwa magerezani kutokana na kukinzana na sheria ilikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 ni 364, mwaka 2013 ni 321, mwaka 2014 ni 373, mwaka 2015 walikuwa ni 334 na mwaka 2016 ni 616. Hivyo kufanya jumla yake wote kuwa ni 2008.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi kutokana na sababu mbalimbali.
(a) Je, ni idadi ya watu wangapi waliopoteza maisha katika Jimbo la Ushetu kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015?
(b) Je, mauaji ya makundi haya yanapungua au yanaongezeka katika Jimbo la Ushetu?
(c) Je, Serikali imeshirikisha vipi jamii kupiga vita mauaji haya, vikiwemo vikundi vya dini, walinzi wa jadi (sungusungu) na uongozi wa kimila Jimboni Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2010 wazee waliouawa walikuwa wawili, mwaka 2011 wazee wanne, mwaka 2013 wazee watano, mwaka 2014 wazee waliouawa walifikia sita, mwaka 2015 walikuwa wawili, mwaka 2016 wawili na mwaka 2017 alikuwa ni mzee moja. Kwa hiyo, jumla ya wazee ambao wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwaka 2010 hadi 2017 ni wazee 22 katika Jimbo la Ushetu. Kwa upande wa walemavu wa ngozi, katika kipindi hicho hakuna mlemavu aliyeuawa wala kujeruhiwa Jimboni Ushetu ila kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka 2010 mpaka 2017 walemavu wa ngozi waliouawa walikuwa ni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mauaji ya makundi haya katika miaka ya karibuni yanapungua kutokana na misako iliyofanywa ya kuwakamata waganga wa kienyeji ambao wanapiga ramli chonganishi na kuchochea imani za kishirikina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukomesha mauaji haya, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kushirikiana na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali ndani na nje ya Jimbo hilo katika kutoa elimu ya ukatili huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikishirikiana na jamii na taasisi za kidini, vikundi vya ulinzi jamii ndani na nje ya Jimbo la Ushetu kwa kuwapa elimu wananchi ili kudhibiti maujai hayo ya kikatili.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA aliuliza:-
Kituo cha Polisi Bububu ni kikongwe sana na pia kimechakaa sana na kinahitaji ukarabati mkubwa. Je, ni lini kituo hicho kitafanyiwa ukarabati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, na mimi naomba niungane na Waheshimiwa wengine kumshukuru Mwenyezi Mungu kukujalia kuungana na sisi leo ukiwa mzima. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Bububu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uchakavu wa vituo vya polisi vikongwe nchini kikiwemo Kituo cha Polisi cha Bububu. Jeshi la Polisi lina mpango wa kuvikarabati vituo hivyo kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, ukarabati wa vituo hivyo vya Polisi kikiwemo Kituo cha Polisi Bububu utafanyika ili kuboresha mazingira ya kazi kwa askari wetu ili kuwawezesha kutoa huduma bora kwa wananchi. (Makofi)
MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:-
• Je, Serikali inatumia pesa kiasi gani kuhudumia mfungwa mmoja kwa siku kwa huduma ya chakula tu?
• Vitendo kama kulala chini, kulala bila blanketi au shuka, kulala bila neti vimekuwa vya kawaida kabisa katika Magereza yetu nchini; je, hii nayo ni sehemu ya adhabu ambayo wafungwa wanapewa kwa mujibu wa sheria?
NAIBU WAZIRI MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edward Franz Mwalongo, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Magereza katika kutekeleza jukumu lake la kuwapokea na kuwahifadhi wahalifu kisheria, pia hutoa huduma ya chakula kwa wahalifu kupitia bajeti inayotengwa na Serikali kila mwaka wa fedha. Gharama ya chakula kwa mfungwa mmoja kwa siku ni wastani wa shilingi 1,342.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za wafungwa na mahabusu Magerezani kwa kununua vifaa mbalimbali vya malazi ikiwemo magodoro, shuka, mablanketi na madawa ya kuua wadudu kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha. Kwa msingi huo inapotokea ukosefu wa huduma hizo, inakuwa siyo sehemu ya adhabu kwa wafungwa bali hutokea kutokana na idadi kubwa ya wafungwa gerezani.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Kuchelewesha haki ni kunyima haki.
Je, Jeshi la Polisi limejitathmini juu ya utendaji wake, hususan katika Idara ya Upelelezi wa Makosa mbalimbali kabla ya kuyafikisha mashtaka mahakamani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, upelelezi wa makosa ya jinai unafanywa kwa kuzingatia sheria mbalimbali kama vile Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai Sura ya 20 Marejeo ya mwaka 2002, Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 Marejeo mwaka 2002 na Sheria ya Ushahidi Sura ya 6 Marejeo ya mwaka 2002, pamoja na kuzingatia kanuni za kiutendaji za Jeshi la Polisi (Police General Orders) na sheria nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya lengo la upelelezi wa makosa ya jinai ni kukusanya ushahidi utakaothibitisha kosa lililotendeka na kuripotiwa kituoni. Aidha, kuna baadhi ya makosa yaliyotendeka huhitaji muda mrefu ili ushahidi wake kuweza kupatikana, mathalani makosa ya mauaji na yanayofanana na hayo. Inapodhihirika kuwa kuna ushahidi uliopatikana unaweza kuthibitisha kosa, jalada hupelekwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa hatua za kusomwa na kuandaa mashtaka pale ambapo wanaona ushahidi umejitosheleza na kupeleka mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi hufanya tathmini ya kutosha katika utendaji wake kupitia Kitengo cha Ndani cha Tathmini na Uangalizi (Internal Monitoring and Evaluation) na kutoka kwa Waangalizi wa Nje (External Oversight) ambao hulisaidia Jeshi la Polisi kurekebisha kasoro mbalimbali za kiutendaji.
MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-
Wilaya ya Chemba haina Kituo cha Polisi; je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Polisi na nyumba za askari?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Nkamia, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Jeshi la Polisi lina uhaba wa vituo vya polisi pamoja na nyumba za kuishi Askari kote nchini ikiwemo Wilaya ya Chemba. Ili kutatua changamoto hii Jeshi la Polisi linashirikisha wadau wa eneo husika pamoja na wadau wengine wa maeneo kwa maendeleo ili kufanikisha azma ya Serikali ya kujenga vituo vya kisasa vya polisi pamoja na nyumba za kuishi askari.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilayani Chemba Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, wananchi na wadau wengine wapo kwenye hatua za awali za kuanza ujenzi wa kituo cha polisi. Aidha, kwa sasa mchoro wa ramani ya kituo na gharama za ujenzi (BOQ) zimeshakamilika na ukusanyaji wa mahitaji ya ujenzi unaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini jitihada hizi zitaungwa mkono na Mheshimiwa Mbunge ili kuhakikishia wananchi wake usalama wao pamoja na mali zao.
MHE. ANDREW J. CHENGE aliuliza:-
Katika miaka ya 1980 wanakijiji wa Kijiji cha Mwanchumu, Salaliya na Matongo walitoa maeneo yao kwa Serikali ili yatumike kwa shughuli za kilimo zilizokusudiwa na Gereza la Matongo lakini kwa sasa maeneo hayo hayatumiwi na Magereza kikamilifu.
Je, Serikali ipo tayari kurejesha eneo hilo ambalo halitumiki kikamilifu kwa wananchi wa vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Andrew John Chenge, Mbunge wa Bariadi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Gereza la Matongo liko Mkoani Simiyu katika Wilaya ya Bariadi na lina ukubwa wa hekari 2472.62. Gereza hili lilianzishwa mwaka 1975 kwa kuchukua eneo lililokuwa la Mbunge wa zamani wa eneo hilo, Marehemu Edward Ng’wani ambapo alifidiwa eneo hilo kwa kupewa eneo lingine na Serikali. Aidha, wananchi wa Vijiji vya Mwanchumu, Salaliya kwa asili ni wahamiaji kutoka maeneo mengine na siyo wenyeji wa Matongo.
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kuwa Serikali iko kwenye mpango wa kuboresha kilimo kupitia Jeshi la Magereza kwa kuliwezesha kuzalisha chakula cha kutosheleza kulisha wafungwa na mahabusu. Eneo la Gereza la Matongo lipo kwenye orodha ya maeneo yaliyopewa kipaumbele katika kilimo cha mahindi, alizeti, pamba, ufugaji wa nyuki na mifugo pamoja na upandaji wa miti na uhifadhi wa mazingira.
Mheshimiwa Spika, Serikali ilitwa eneo hilo ili kuwezesha Magereza kuendeleza shughuli za urekebishaji wafungwa kwa kutumia kilimo cha ufugaji ambapo mazao mbalimbali ya kilimo hustawi. Kwa sasa eneo hilo limeshapimwa na taratibu za kufuatilia upatikanaji wa hati unaendelea.
Mheshimiwa Spika, kutokana na eneo hilo kuwa kwenye mpango mkakati wa Jeshi la Magereza wa kujitosheleza kwa chakula na shughuli nyingine, Serikali haina mpango wa kulirejesha eneo hilo kwa vijiji tajwa.
MHE. TWAHIR AWESU MOHAMED aliuliza:-
Jeshi la Polisi lina dhamana kubwa ya kulinda usalama wa raia na mali zao na ni msimamizi mkuu katika haki za binadamu:-
(a) Je, ni lini Jeshi hilo litafanya kazi zake kisayansi zaidi na kuondokana na kutumia nguvu zisizo za lazima wakati wa kutekeleza majukumu yake?
(b) Je, suala la weledi kwa watendaji wa polisi linasimamiwa vipi ili polisi waweze kupambana na uhalifu unaokua kitalaam kila siku?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Twahir Awesu Mohamed, Mbunge wa Mkoani lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi ni chombo kilichoanzishwa kwa mujibu wa Katiba kusimamia usalama wa raia na mali zao na katika utendaji wake linaongozwa na sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali. Aidha, Jeshi la Polisi limejiwekea kanuni za kudumu (PGO) ambazo zimetafsiri na kutoa mwongozo wa utekelezaji wa sheria zote zinazoongoza utendaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa kazi zake askari anaruhusiwa kutumia nguvu inayoendana na mazingira ya tukio. Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kifungu namba 11(2) kinamruhusu askari kutumia nguvu katika ukamataji iwapo mkamatwaji atakaidi. Pia PGO 274 inaeleza mazingira ya matumizi ya nguvu na aina ya nguvu inayopaswa kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiwajengea uwezo wa kiutendaji askari kwa kutoa mafunzo mbalimbali sehemu za kazi yenye lengo la kuwakumbusha taratibu za kazi, pia limekuwa likitoa mafunzo ya weledi ya ndani na nje ya nchi ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha linafanya kazi zake kwa weledi Jeshi la Polisi limekuwa likiajiri wasomi wenye taaluma mbalimbali kama vile TEHAMA, maabara, uchunguzi wa nyaraka na taaluma zingine zinazohusiana na makosa yanayosababishwa na ukuaji wa teknolojia.
MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS aliuliza:-
Kituo cha Polisi cha Mkokotoni kiliungua mnamo tarehe 27/12/2010 na ujenzi wake ulianza mara moja.
Je, ni lini ujenzi huu utakamilika na kituo hicho kuendelea na shughuli zake?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Haji Khamis, Mbunge wa Nungwi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa kituo cha polisi cha Mkokotoni kilipata ajali ya moto mwaka 2010. Baada ya kuungua kwa kituo hichi, wananchi wa eneo husika waliendelea kupata huduma za kipolisi kupitia jingo lililokuwa pembeni na kituo kilichoungua moto. Serikali kupitia Jeshi la Polisi ilitafuta mkandarasi ambaye alianza kujenga upya kituo hicho na kwa sasa ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 80. Aidha, shughuli za Kituo cha Polisi cha Mkokotoni zitaanza katika jengo jipya baada ya kukamilika kwa ujenzi wake.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi Wilaya ya Mlele?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uhitaji wa vituo vya polisi pamoja na nyumba za kuishi askari kote nchini ikiwemo Wilaya ya Mlele. Ili kutatua changamoto hii, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inashirikisha wananchi pamoja na wadau mbalimbali wengine wa maendeleo ili kufanikisha azma ya Serikali ya kujenga vituo vya polisi vya kisasa nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ufinyu wa bajeti na uhitaji wa vituo vya polisi katika maeneo mbalimbali nchini kuwa mkubwa, namwomba Mheshimiwa Mbunge kushiriki katika jitihada hizi kwa kuhamasisha wananchi wake kushiriki katika mpango huu ili kuhakikisha huduma za Kipolisi zinaimarika karika eneo hilo. (Makofi)
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Wilaya ya Itilima haina Kituo cha Polisi cha Wilaya. Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Itilima?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi lina jumla ya Wilaya za Kipolisi 168 nchi nzima ambapo kati ya hizo, Wilaya 127 zina majengo kwa ajili ya Ofisi na Vituo vya Polisi vya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhaba wa vituo vya polisi pamoja na nyumba za kuishi askari nchini umesababishwa na kukosekana kwa rasilimali za kutosha kukidhi mahitaji ambayo ni makubwa. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi linafanya jitihada mbalimbali kama vile kutumia rasilimali zilizopo katika eneo husika pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ili kukabiliana na tatizo la uhaba wa vituo vya polisi nchini. (Makofi)

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-
Moja ya majukumu makubwa ya Serikali ni kulinda raia na mali zao kupitia vyombo vyake vya ulinzi na usalama ikiwemo Polisi:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kukirejesha Kituo cha Polisi katika Tarafa ya Kipatimu Wilayani Kilwa ambacho kilihamishwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Kituo cha Polisi cha Kipatimu kilifungwa mwaka 1998 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo uchakavu wa miundombinu na mahusiano mabaya kati ya raia na Askari kiasi cha kutishia usalama wa Askari na mali za Serikali zilizoko kituoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa wananchi wameona umuhimu wa kurejesha huduma za Polisi katika eneo husika ambapo wameanza ujenzi wa kituo kipya cha Polisi. Aidha, nimshauri Mheshimiwa Mbunge kuwasiliana na Jeshi la Polisi Mkoa wa Lindi ili kuona namna bora ya kukamilisha ujenzi wa kituo hicho.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kukipatia Kituo cha Chanika gari la patrol?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikabe Waitara, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kipolisi ya Ukonga ipo katika Mkoa wa Kipolisi Ilala na Kituo Kikuu ni Kituo cha Polisi Stakishari ambacho kinasaidiwa na vituo vingine vidogo kama vile Pugu, Chanika, Msongola, Gongolamboto, Mazizini, Karakata, Kinyerezi, Tembo Mgwaza na Kitunda. Vituo hivi vyote huhudumiwa kwa magari saba toka katika Kituo cha Stakishari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha katika Kituo cha Polisi cha Chanika lipo gari Na. PT 1889 Toyota Land Cruiser Pickup, ndilo hutumika kufanya doria katika eneo hilo likisaidiwa na magari mengine toka katika Kituo cha Stakishari, kwani kituo hiki ni kikubwa ukilinganisha na vituo vingine vilivyotajwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi litaangalia uwezekano wa kuongeza gari katika Kituo cha Polisi Chanika na kuzingatia vigezo kama vile hali ya uhalifu, idadi ya watu, sababu za kiutawala na kijiografia kwa kulinganisha na maeneo mengine yenye mahitaji kama haya.
MHE. MGENI JADI KADIKA aliuliza:-
Vituo vingi vya Polisi havina miundombinu mizuri na vingine ni vibovu na vichakavu:-
Je, ni lini Serikali itakifanyia maboresho Kituo cha Polisi Konde?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa miundombinu ya Kituo cha Polisi Konde ni mibovu na imechakaa kama ilivyo katika maeneo mengine nchini. Serikali kupitia Jeshi la Polisi itaendelea kufanya ukarabati wa vituo hivyo kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukarabati wa Kituo cha Polisi Konde, utafanyika mara fedha zitakapopatikana ili kuboresha mazingira ya kazi kwa askari wetu na kuwawezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-
Tatizo la wahamiaji haramu hasa kutoka Ethiopia limeshamiri sana katika nchi yetu kwa sasa:-
(a) Je, ni wahamiaji haramu wangapi wamekamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria?
(b) Kama wapo ambao wanaendelea na kifungo, je, ni hatua gani za kisheria ambazo zinachukuliwa baada ya kutolewa kifungoni?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) yote kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Uhamiaji imekamata jumla ya wahamiaji haramu 13,393 katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi 2018. Miongoni mwao wahamiaji haramu 2,815 walishtakiwa, 117 walitozwa faini, 429 walifungwa, 6,316 waliondoshwa nchini, 1,353 waliachiwa huru baada ya kutoa nyaraka za uthibitisho wa ukaazi wao. Aidha, zipo kesi 2,363 zinazoendelea katika mahakama mbalimbali nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za kisheria ambazo huchukuliwa baada ya wahamiaji haramu kumaliza vifungo vyao gerezani ni kurudishwa nchini kwao.
MHE. LUCIA M. MLOWE (K.n.y. MARY D. MURO) aliuliza:-
Kumekuwepo na mkanganyiko wa watumishi wa zimamoto kwenye viwanja vya ndege na viwanja hivyo kutokuwa huru katika kuwatumia kutokana na kuwa si sehemu ya waajiri wao:-
Je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha viwanja vinajitegemea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linasimamiwa na Sheria Namba 14, Sura ya 427 ya Mwaka 2007 iliyounganishwa Vikosi vya Zimamoto vilivyokuwa chini ya TAMISEMI na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kuwa chini ya Kamandi moja ya Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ni Taasisi za Serikali ambazo hufanya kazi kwa pamoja kwa lengo la kutoa huduma ya kulinda mipaka ya nchi, hivyo hakuna mkanganyiko wowote wa kiutendaji. Hata hivyo, naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa upo ushirikiano mzuri kati ya vyombo hivi vya ulinzi na usalama na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege katika kutekeleza majukumu yao.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA aliuliza:-
Je, lini Serikali itapeleka gari, radio call pamoja na vitendea kazi vingine katika Kituo cha Polisi cha Chwaka na Jozani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bhagwanji Maganlal Meisuria, Mbunge wa Chwaka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uhaba wa magari pamoja na vitendea kazi katika Vituo vya Polisi nchini kikiwemo Kituo cha Polisi Chwaka na Jozani. Hata hivyo, Jeshi la Polisi linaendelea na mchakato wa upatikanaji wa magari mapya yaliyonunuliwa na Serikali. Baada ya mchakato huu kukamilika, hatua za kuyagawa zitafuata kwa kuzingatia kiwango cha uhalifu katika maeneo husika, idadi ya watu na ukubwa wa eneo la doria.
Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi Chwaka kinatumia mawasiliano ya radio ya mezani kwa sababu umbali wa ilikofungwa mitambo ya mawasiliano ya radio za mkononi. Aidha, radio za mezani kwa ajili ya Kituo cha Polisi Jozani imekwishapatikana na mafundi wa Radio za Polisi wanamalizia ufungaji wake ili kurejesha mawasiliano ya uhakika katika eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kuwa inaboresha mawasiliano katika vituo vyote vya Polisi nchini kwa kutafuta repeaters (mitambo wa radio za mkononi) ambazo zitafungwa katika vituo visivyokuwa na mawasiliano ya radio za mkononi ikiwemo Chwaka na Jozani.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE aliuliza:-
Mkoa wa Singida unakua kwa kasi sana na ujenzi wa majengo makubwa ya kisasa umeongezeka, lakini kwa muda mrefu sasa hakuna gari la zimamoto linaloweza kuhudumia mkoa; gari lililopo kwa sasa ni bovu na lina ujazo wa lita 1,500 tu na lenye ujazo wa lita 7,000 lilipata ajali miaka iliyopita na Serikali iliahidi kulifanyia matengenezo lakini mpaka sasa haijafanya hivyo:-
Je, ni lini Serikali itapeleka gari la kisasa la zimamoto Mkoani Singida ili kukabiliana na majanga ya moto yanayoweza kutokea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aisharose Matembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Mkoa wa Singida unakua kwa kasi ingawa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lina gari moja lenye ujazo wa lita 1,500 ambalo linafanya kazi zake na gari la pili ni bovu. Hata hivyo, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linatarajia kulifanyia matengenezo gari la pili ambalo ujazo wake ni lita 7,000 na pindi fedha zitakapopatikana gari zote mbili zitaweza kufanya kazi kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuimarisha shughuli za zimamoto na uokoaji, Serikali kwa kupitia bajeti ya mwaka 2018/2019, imepanga kununua gari tano za zimamoto ambazo zitagawiwa katika maeneo mbalimbali nchini yenye uhitaji mkubwa. Aidha, Wizara inaandaa marekebisho ya Sheria ya Zimamoto na Uokoaji Namba 14 ya Mwaka 2017 ili kuzitaka halmashauri za manispaa, miji na wilaya kununua magari ya kuzimia moto ili kuondokana na upungufu mkubwa wa magari uliopo hivi sasa.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA (K.n.y. MHE. BUPE MWAKANG’ATA) aliuliza:-
Vijana wengi wamejiajiri katika shughuli mbalimbali ikiwemo waendesha bodaboda, lakini waendesha bodaboda hao wamekuwa wakisumbuliwa sana na askari wa barabarani kwa kutozwa faini ambazo muda mwingine hazina maana na hivyo kuwakatisha tamaa.
Je, Serikali inachukua hatua gani ili kudhibiti vijana hawa wasinyanyaswe?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mchango mkubwa wa biashara ya pikipiki kwa huduma ya usafiri kwa jamii ambapo vijana wengi wamepata ajira hivyo kukuza kipato chao. Umuhimu mkubwa wa usafiri huu hauwaondolei wahusika wa usafiri huu wajibu wa kuzingatia Sheria na Kanuni za Usalama Barabarani ili kuufanya usafiri huu kuwa salama kwa watumiaji.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Jeshi la Polisi litaendelea kuwachukulia hatua wale wote ambao wanakiuka Sheria na Kanuni za usalama barabarani, ni rai yangu kwa wale wote ambao wanahisi kuonewa ama kunyanyaswa wakati wakitumia usafiri huu kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ama Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU) aliuliza:-
Gereza la Wilaya ya Igunga linakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo ukosefu wa ngome, hakuna Ofisi za Mkuu wa Gereza na Utawala, hakuna nyumba za askari lakini pia gereza hilo ni dogo na linahudumia wafungwa na mahabusu wa kiume tu, wafungwa na mahabusu wa kike hupelekwa Gereza Wilaya ya Nzega.
Je, ni lini Serikali itajenga Gereza la Wilaya ya Igunga ili liweze kutoa huduma bora kwa wafungwa mahabusu Wilayani Igunga?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa gereza la mahabusu Wilaya ya Igunga ulianza mwaka 2003 ili kuwapokea na kuwahifadhi mahabusu na wafungwa kutoka Wilaya ya Igunga ambao walikuwa wakipelekwa na kuhifadhiwa katika Gereza la Nzega ambalo nalo ni dogo na hivyo kusababisha msongamano mkubwa. Ujenzi huo bado haujakamilika kwani unafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa gereza hilo utakapokamilika kutakuwa na maeneo yote muhimu yanayotakiwa kwenye gereza kama vile ngome, ofisi, mabweni ya wafungwa na mahabusu, jiko, bwalo la chakula na litakuwa na uwezo wa kuhifadhi wafungwa na mahabusu wa jinsia zote.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi katika Wilaya mpya ya Buhigwe na kutoa vitendea kazi kwa Jeshi la Polisi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Albert Obama Ntabaliba, Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto za miundombinu Kijiografia pamoja na nyinginezo zinazoikabili pamoja na mikoa mipya hapa nchini. Changamoto hizi ni pamoja na uhaba wa Ofisi na nyumba za kuishi watumishi. Hata hivyo, Jeshi la Polisi katika Wilaya mpya ya Buhigwe limeshatenga eneo kwa ajili ya Ofisi ya Mkuu wa Polisi wa Wilaya na Kituo cha Polisi cha Wilaya chenye ukubwa wa ekari tano. Pia zimetengwa ekari 20 kwa ajili ya nyumba za makazi ya Askari Polisi. Aidha, kwa sasa huduma za kipolisi katika maeneo ya Buhigwe hutolewa kupitia kituo kidogo cha Polisi cha Buhigwe na Manyovu.
Mheshimiwa Spika, mahitaji ya vituo vya polisi pamoja na nyumba za makazi ya askari nchini ni makubwa na yanahitaji fedha nyingi. Haya hivyo, Jeshi la Polisi limeweka vipaumbele katika Mikoa na Wilaya mpya, Miji inayokuwa kwa kasi pamoja na maeneo yenye viashiria na matishio ya kiusalama ili kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-
Polisi wanapowakamata watuhumiwa baadhi wanawaweka ndani kwa saa 24 na wengine zaidi ya saa 24.
• Je, ni makosa yapi mtuhumiwa anaweza kuwekwa ndani zaidi ya masaa 24?
• Je, ni makosa yapi ambayo mtuhumiwa anaweza kuwekwa ndani chini ya saa 24?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20, kifungu cha 148(5)(a) mpaka (e) kinaeleza makosa mabayo mtuhimiwa anaweza kuwekwa kizuizini zaidi ya saa 24. Makosa hayo ni kama vile uhaini, mauaji, ujambazi wa kutumia silaha, kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya, ugaidi, usafirishaji wa fedha haramu, mtuhumiwa aliyewahi kuhukumiwa kifungo kinachozidi miaka mitatu ama aliwahi kuruka dhamana na mengineyo.
Mheshimiwa Spika, makosa ambayo mtuhumiwa anaweza kuwekwa ndani chini ya saa 24 ni makosa yote isipokuwa yaliyoainishwa katika kifungu cha 148(5)(a) mpaka (f).
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Jeshi la Polisi kupitia IGP Ernest Mangu ambaye alifanya ziara Wilayani Kahama mapema mwezi Agosti, 2016 alitangaza kuanzisha Mkoa mpya wa Kipolisi wa Kahama na Wilaya za Kipolisi za Msalala, Ushetu na Kahama; na wilaya hizo mpya za kipolisi zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa askari na vitendea kazi vyao hasa vyombo vya usafiri:-
i. Je, ni watumishi wangapi wamepangwa Wilaya mpya ya Kipolisi ya Msalala?
ii. Je, Serikali iko tayari kusaidia vyombo vya usafiri hasa magari na pikipiki Wilaya ya Kipolisi ya Msalala?
iii. Je, Serikali imejipangaje kujenga ofisi za polisi wilaya na nyumba za makazi kwa askari katika Wilaya za Msalala, Ushetu na Kahama Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uhitaji wa huduma ya kipolisi katika maeneo ya Ushetu, Msalala na Kahama. Aidha, maombi ya Msalala kuwa Wilaya ya Kipolisi yameshakamilika na maombi ya Kahama kuwa Mkoa wa Kipolisi yanaendelea kuzingatiwa. Kwa sasa Wilaya ya Msalala ina jumla ya maofisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali 57.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nia ya Serikali kuona kuwa vitendea kazi kwa Jeshi la Polisi vinapatikana ili kurahisisha utoaji wa huduma za polisi kwa wananchi. Wilaya mpya ya Msalala imepatiwa mgao wa gari moja jipya na taratibu za usajili zitakavyokamilika gari hilo litapelekwa Msalala kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Msalala, Ushetu na kahama Mjini ni miongoni mwa wilaya 65 nchini ambazo hazina majengo ya vituo vya polisi vyenye hadhi ya wilaya. Hata hivyo, halmashauri ya wilaya imeshatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa kituo na makazi ya askari na ujenzi utaanza mara pale fedha zitakapokuwa zimepatikana.
MHE. ZAYNAB M. VULLU (K.n.y. MHE. MAULID S. MTULIA) aliuliza:-
Serikali inafanya juhudi kubwa ya kuzuia biashara ya ukahaba kwa kuwakamata wauzaji na wanunuzi na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria. Pamoja na jitihada hizo bado biashara hiyo haramu inaendelea kwa kasi ileile:-
Je, Serikali ina mpango gani mbadala wa kuzuia biashara hii haramu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Said Mtulia, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikipambana na watu wanaojihusisha na vitendo vya ukahaba nchini. Jeshi la Polisi limekuwa likifanya misako kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kwa kubaini na kukamata watu ambao wanajihusisha na vitendo hivyo ambavyo ni kinyume na maadili ya Kitanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ukahaba ni suala mtambuka ambapo kulikabili kunahitaji ushirikiano wa wadau wengi. Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kupitia Jeshi la Polisi, imeandaa mkakati wa kushirikisha taasisi nyingine za Serikali kama vile TAMISEMI, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii na kupunguza hatimaye kumaliza vitendo hivi ambavyo vinautia doa utamaduni wa nchi yetu. Aidha, mkakati huu unahusisha ujenzi, kutoa elimu ya madhara ya ukahaba, faida za ujasiriamali na kuwashirikisha viongozi wa dini katika kufundisha maadili.
MHE. SAED A. KUBENEA aliuliza:-
Kumekuwepo na vitendo vingi vya uhalifu hapa nchini kwa watu kuvamiwa, kupigwa, kujeruhiwa na kuporwa mali zao na hata kuuawa:-
• Je, Serikali ina mpango gani wa kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu ambavyo vinatishia usalama wa raia na mali zao?
• Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza juhudi za ulinzi wa raia na mali zao ili kudumisha amani na utulivu nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saed Ahmed Kubenea, Mbunge wa Ubungo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
i. Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi ina mipango mbalimbali ya kukomesha vitendo vya uhalifu kwa kuimarisha doria za miguu, pikipiki na magari, pia kufanya misako dhidi ya uhalifu na wahalifu. kutoa elimu kwa jamii kuhusu mbinu za kukabiliana na uhalifu, kufanya operation za mara kwa mara na kushirikisha jamii kwenye ulinzi wa maeneo yao kupitia dhana ya Polisi Jamii.
ii. Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kufanya juhudi za kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao kwa kuendelea kuajiri askari na kuongeza vitendea kazi pia, kwa kutumia falsafa ya kugatua madaraka. Serikali imeshapeleka wakaguzi katika tarafa, jimbo, kata, shehiya ili kushiriki kikamilifu kwa kuyabaini maeneo tete ambayo huwa ni vyanzo vya uhalifu.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Wananchi wa Kijiji cha Luganzu na majirani zao wa Ntumagu wanakabiliwa na adha kubwa ya matukio ya ujambazi pamoja na ukosefu wa Kituo cha Polisi kijijini hapo kwa ajili ya kuimarisha ulinzi. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu hali hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Luganzu na Ntumagu kama yalivyo maeneo mengine ya nchi kumekuwa na uhalifu mdogo na wa kawaida katika siku za hivi karibuni na hakuna tukio lolote kubwa la ujambazi ambalo limeripotiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kijiografia Vijiji vya Luganzu na Ntumagu vipo katika vituo vikubwa vya polisi vya operation vya Nyakanazi, Kalenge na Kakongo ambavyo hufanya doria za magari ya mara kwa mara katika kudhibiti uhalifu. Hali hii imepelekea wahalifu kukimbilia katika vijiji tajwa hivyo kuleta hofu na wasiwasi kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kudhibiti Jeshi la Polisi limefungua kituo kidogo cha polisi katika kijiji cha Ntumagu ili kudhibiti njia ya wahalifu waliokuwa wakiingia vijijini kutokea maeneo ya Nyakanazi, Kalenge na Kakongo walikodhibitiwa.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Gereza la Kilimo la Mng’aro ni miongoni mwa magereza kongwe hapa nchini, lakini gereza hili limekuwa na miundombinu chakavu kutokana na umri wake:-
Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kulifanyia ukarabati mkubwa gereza hili pamoja na kuongeza uwezo wa kuchukua wafungwa wengi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Gereza la Kilimo la Mng’aro miundombinu yake ni chakavu kutokana na gereza hilo kuwa la muda mrefu, tangu mwaka 1977 hali ambayo inasababisha gereza hilo pamoja na miundombinu yake kuwa chakavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo Serikali linatekeleza mpango wa muda mrefu kwa nchi nzima wa kuboresha majengo hayo kwa kuyafanyia ukarabati mkubwa, ikiwemo Gereza la Mng’aro ili kuimarisha, kuyaboresha na kuyafanyia upanuzi.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Moja ya jukumu la Serikali ni kuhudumia wafungwa kwa maana ya kukwapatia huduma za msingi kama vile chakula, mavazi na matibabu:-
Je, Serikali inafanya nini ili kuhakikisha huduma hizo za msingi katika Gereza la Kasulu zinapatikana kwani wana hali mbaya sana hasa kimavazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, huduma za wafungwa magerezani hujumuisha chakula, mavazi, matibabu pamoja na huduma nyingine muhimu ambazo hutengewa fedha katika bajeti ya Serikali ya kila mwaka. Ili kupunguza tatizo la uchakavu wa sare za wafungwa kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi milioni mia sita kwa ajili ya kushona sare za wafungwa nchi nzima. Aidha, kwa mwaka 2018/2019, Serikali imetenga shilingi milioni mia moja kwa ajili ya sare za wafungwa nchi nzima.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE (K.n.y. MHE. DANIEL NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma hususan Wilaya za Kasulu na Kibondo zimekuwa makazi ya wakimbizi kwa muda mrefu sana.
Je, ni lini Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na UNHCR itakuja na mpango kabambe wa kusaidia maeneo yaliyoathiriwa na ujio wa wakimbizi hao (a comprehensive plan and support for refugee affected areas)?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli baadhi ya maeneo ambayo hupokea wakimbizi nchini hupata athari mbalimbali ikiwemo uharibifu wa mazingira. Hata hivyo, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) inatekeleza mipango mbalimbali inayolenga kuboresha huduma kwenye jamii katika Wilaya zinazohifadhi wakimbizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Wilaya za Kibondo na Kasulu huduma ambazo zimekuwa zikiboreshwa ni pamoja na afya, elimu, kilimo, masoko, ujasiriamali pamoja na hifadhi ya mazingira.
MHE. SUSANNE P. MASELE aliuliza:-
Wananchi wakazi wa Kijiji cha Ishokelahela, Misungwi, Mwanza, wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya kihalifu, kinyama na kikatili na Vyombo vya Dola kuwaondoa katika makazi yao na kuacha kuchimba dhahabu ili eneo hilo libaki kwa Mwekezaji anayetaka kuwaondoa kwa nguvu kinyume cha sheria:-
i. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu vitendo hivyo wanavyofanyiwa wananchi hao?
ii. Je, Serikali iko tayari kuunda timu kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa mgogoro huo na kuchukua hatua stahiki ambazo zitamaliza kabisa mgogoro na kuwawajibisha wote ambao wamesababisha hali iliyopo sasa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susanne Maselle, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kijiji cha Ishokelahela ambao ni wachimbaji wadogo wadogo wa dhahabu wamekuwa na mvutano na Mwekezaji Isinka Federation 2014 Mining Cooperative and Society Limited anayefanya shughuli za uchimbaji wa dhahabu katika eneo hilo kihalali. Mvutano huo umepelekea wananchi hao kutaka kuvamia eneo la Mwekezaji huyo bila kufuata sheria kitendo ambacho kinaweza kusababisha uvunjifu wa amani katika eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linao wajibu wa kuhakikisha hali ya ulinzi na usalama inaimarishwa katika eneo hilo kwa mujibu wa sheria, hivyo haliwezi kuruhusu wananchi kuchukua sheria mkononi na kuvamia eneo hilo ambalo linamilikiwa kihalali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, si kweli kwamba vyombo vya dola vimekuwa vikiwanyanyasa na kuwafanyia unyama wa kikatili wananchi katika makazi yao bali katika eneo husika Jeshi la Polisi limekuwa likiwazuia kuingia katika eneo ambalo sio mali yao kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala hili ni suala muhimu, hata hivyo, Serikali inaendelea kulifuatialia kwa karibu na kutafuta suluhisho la kudumu ili kuondoa migongano ambayo inaweza kuhatarisha amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nitumie fursa hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge awahamasishe na kuwashauri wananchi wa Kijiji hicho ambao ni wachimbaji wadogo wadogo kuungana katika vikundi na kuomba leseni za uchimbaji ili wafanye shughuli zao kihalali.
MHE. HAWA A. GHASIA (K.n.y. MHE. RASHIDI M. CHUACHUA) aliuliza:-
Jeshi la Polisi katika Wilaya ya Masasi halina nyumba za makazi na usafiri kwa muda mrefu sana:-
a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea askari hao nyumba za kuishi kwa sababu nyumba wanazoishi sasa zimechakaa sana na pia hazitoshelezi mahitaji yao?
b) Je, ni lini Serikali itawapatia usafiri wa uhakika Askari hao ili waweze kusimamia usalama wa raia na mali zao kwa uhakika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la uhaba wa nyumba za makazi kwa Askari wa Jeshi la Polisi nchini ikiwemo Wilaya ya Masasi. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ili kupunguza tatizo la makazi ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wananchi na wadau kujenga nyumba kwa ajili ya makazi ya Askari.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali itajenga nyumba za kuishi Askari kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Wilaya ya Masasi ina magari matatu ambapo kati ya hayo magari mawili ni mabovu. Jeshi la Polisi hugawa magari kwa kuzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo hali ya uhalifu, sababu za kiutawala na jiografia ya mahali husika. Kwa kuzingatia vigezo hivyo hususani jiografia yake, Wilaya ya Masasi itapewa kipaumbele katika mgao wa magari mara yatakapopatikana.
MHE. MUSSA R. NTIMIZI aliuliza:-
Wananchi Halmashauri ya Wilaya ya Tabora kwa kushirikiana na Mbunge wamejenga kituo kikubwa cha Polisi katika Kata ya Loya kilichogharimu zaidi ya Sh.100,000,000/= lakini mpaka sasa hakijaanza kufanya kazi:-
• Je, Serikali ipo tayari kutenga bajeti kusaidia ujenzi wa nyumba za askari na kurekebisha upungufu mbalimbali uliopo?
• Je, Serikali ipo tayari kutoa gari jipya ili kusaidia kurahisisha kazi ya Ulinzi na Usalama katika eneo hilo kwani kituo hicho kipo kilomita 120 kutoka Makao Makuu ya Wilaya – Isikizya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Igalula, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi itatenga fedha kwa ajili ya kumaliza Kituo cha Polisi cha Kata ya Loya ambapo nyumba, chumba cha kuhifadhi Mahabusu na chumba cha kuhifadhi silaha vitaimarishwa ili kituo hicho kianze kutoa huduma kwa wananchi. Aidha, napenda kutoa pongezi kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Wananchi pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwa kufanikisha ujenzi wa kituo hicho cha Polisi katika Kata ya Loya.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Uyui ambayo Makao Makuu yake yapo Kata ya Isikizya ina magari matatu na moja ni bovu ambalo linahitaji matengenezo. Serikali inaendelea na mchakato wa kutafuta magari kwa ajili ya Jeshi la Polisi na pindi yatakapopatikana yatagawiwa katika maeneo mbalimbali yenye mahitaji nchi nzima.
MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-
Kwa muda mrefu kumekuwepo na tatizo kubwa la hali ya usalama katika Jimbo la Ngara tangu mwaka 1993 kutokana na kuwa mpakani mwa nchi za Rwanda na Burundi ambapo kuna mwingiliano mkubwa wa wageni/wahamiaji haramu kutoka nchi hizo.
(a) Je, ni lini Serikali itaanzisha Kanda Maalum ya Kipolisi katika Wilaya ya Ngara ili kudhibiti hali ya usalama?
(b) Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya polisi katika Kata ya Mabawe, Muganza, Kirushya, Mtobeye, Mbuba na Nyakisasa?
(c) Kwa kuwa Jeshi la Polisi Wilayani Ngara lina gari moja tu zima na lingine bovu bovu, je, ni lini Serikali itatupatia angalau magari mawili, moja kwa ajili ya Tarafa ya Rulenge na la pili kwa ajili ya Tarafa ya Murusagamba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alex Gashaza, Mbunge wa Ngara lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, hali ya usalama katika Jimbo la Ngara kwa sasa imeimarika ikilinganishwa na miaka iliyopita. Wilaya ya Ngara imepakana na nchi jirani za Rwanda na Burundi. Serikali imeweka mikataba ya ujirani mwema na nchi za Rwanda ambapo Jeshi la Polisi hufanya doria za pamoja mipakani.
Mheshimiwa Spika, kuna changamoto katika mipaka yetu na nchi ya Burundi inayotokana na kukosekana kwa amani katika nchi hiyo na kupelekea watu kuvuka mipaka. Aidha, Jeshi la Polisi nchini limeanzisha vituo vya ulinzi shirikishi ili kujenga uhusiano wa pamoja na wananchi ili kuimarisha hali ya usalama katika eneo hilo. Kwa sasa hali ya usalama katika eneo hilo imeimarika na hakuna haja ya Serikali kuanzisha Kanda Maalum ya Kipolisi.
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la uhaba wa vituo vya Polisi katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Ngara na katika Kata za Mabawe, Muganza, Kirushya, Mtobeye, Mbuba na Nyakisasa. Aidha, katika Kata ya Muganza kitajengwa Kituo cha Polisi eneo la Mkalinzi kwa nguvu za wananchi ambapo katika Kata za Mabawe, Mtobeye, Mbuba na Nyakisasa Polisi hutoa huduma kupitia Vituo Maalum vya Operesheni vya maeneo ya Murugyagira, Rulenge, Kabanga na Bugaramo. Hata hivyo, Serikali itajenga vituo vya polisi katika maeneo hayo kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA aliuliza:-

Kituo cha Polisi Chwaka na Kituo cha Polisi Jozani vina tatizo kubwa la gari la kufanyia doria na ulinzi:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia upatikanaji wa magari mawili kwa Vituo hivyo katika bajeti ya 2018/2019?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bhagwanji Maganlal Meisuria, Mbunge wa Chwaka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Chwaka na Kituo cha Polisi Jozani vipo katika Mkoa wa Kusini Unguja. Tayari Mkoa wa Kusini Unguja umeshapatiwa magari mawili aina ya Ashock Leyland – Trooper na Sauvana kwa ajili ya kusaidia utendaji kazi wa Polisi Mkoani humo ikiwemo doria.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi bado linaendelea kupokea magari mapya kupitia mkataba wa magari 777 kutoka Kampuni ya Ashock Leyland Limited ya India. Hivyo kutokana na hitajio kubwa la rasilimali ya magari lililopo katika mikoa yote ikiwemo Mkoa wa Kusini Unguja na Jimbo la Chwaka, Jeshi la Polisi litaendelea kugawa magari katika mikoa kwa kadri magari yatakavyopatikana na kwa kuzingatia vipaumbele ambavyo ni kiwango cha uhalifu katika maeneo husika na ukubwa wa maeneo ya doria.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:-

Kuna harufu mbaya inayotoka kwenye chumba cha Mahabusu katika Kituo cha Polisi Mazizini Zanzibar na kuwa kero kwa Askari na wananchi wanaofika kupata huduma kituoni hapo.

Je, ni lini Serikali itakifanyia ukarabati kituo hicho ili kuondoa harufu hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bi. Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa hali ya jengo la Kituo cha Polisi Mazizini hairidhishi. Kwa kutambua hilo, Serikali ikishirikiana na wadau wa usalama inaendelea na ujenzi wa Kituo kipya cha Polisi cha kisasa katika eneo la Chukwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jengo hili jipya lipo katika hatua za mwisho za umaliziaji na mara ujenzi utakapokuwa umekamilika shughuli za kiusalama za Jeshi la Polisi za Kituo Kikuu cha Wilaya ya Magharibi ‘B’ katika Mkoa wa Mjini Magharibi zitahamishiwa kutoka Kituo cha Mazizini na kwenda Chukwani.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-

Wafungwa wakimbizi toka nchi za Burundi na DRC wamekuwa wakijaza mahabusu na magereza yetu:-

(a) Je, kwa nini Serikali isikubaliane na nchi za Burundi na DRC kubadilishana wafungwa ili wakimbizi hao wafungwe katika nchi zao?

(b) Je, wafungwa wa aina hiyo wanapokuwa mahabusu na magereza, Shirika la UNHCR linachangia gharama kwa kiasi gani?

(c) Je, UNHCR imechangia fedha kiasi gani kwa wafungwa wakimbizi waliofungwa au kuwekwa mahabusu nchini kuanzia mwaka 2017/2018?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nichodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Mwenyekiti, suala la kubadilishana wafungwa baina ya nchi moja na nyingine huongozwa na mkataba wa makubaliano ulioingiwa baina ya nchi moja na nyingine. Lengo la mkataba huo ni kumpa fursa mfungwa anayetumikia kifungo chake gerezani kutumikia sehemu ya kifungo chake kilichobaki katika nchi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ieleweke kuwa ni utamaduni wa kisheria duniani kwamba mahabusu na mfungwa bila kujali kama ana hadhi ya ukimbizi, wanapopokelewa na kuhifadhiwa katika magereza, jukumu la kuwatunza hufanywa na Serikali ya nchi husika. Serikali yetu imekuwa ikifanya hivyo kwa kufuata Sheria na Kanuni za Magereza zilizopo ambazo kimsingi zimeipa Serikali jukumu hilo. Aidha, ifahamike kuwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Magereza hakuna mahabusu au mfungwa mkimbizi kwani wahalifu wote hupokelewa kwa hati kutoka Mahakama zetu zenye utambulisho wa hadhi ya mahabusu au mfungwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, kwa misingi hiyo suala la Shirika la UNHCR kuchangia gharama za kuwatunza wafungwa na mahabusu wanaodaiwa kuwa ni wakimbizi huwa halipo na halifanyiki kwa sababu kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Magereza zilizopo hazijaainisha kumtambua mahabusu au mfungwa mkimbizi katika magereza yetu.
MHE. LUCY S. MAGERELI aliuliza:-

Tangazo la Serikali Namba 257 kifungu cha 6 kinaelekeza faini za makosa ya barabarani kulipwa kwa Askari aliyeandika faini au kwa OCD au Ofisi ya Mhasibu aliyeko karibu. GN hiyo imetoa nafasi ya kulipa ndani ya siku saba (7) na iwapo faini haitalipwa ndani ya siku saba (7) mkosaji atafikishwa Mahakamani ndani ya siku 10:-

(a) Kwa nini Askari wa Usalama Barabarani huamua kushikilia magari ya wanaokamatwa wakati huohuo, wakati sheria inasema walipe ndani ya siku saba (7)?

(b) Katika Mkoa wa Dar es Salaam kuna mashine za kielektroniki (POS) za kulipia faini na ANPR ambayo husaidia kufuatilia ambao wanakwepa kulipa faini walizoandikiwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza upatikanaji wa POS na ANPR ili kuepusha mifarakano na usumbufu unaojitokeza?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba kifungu cha 6 cha Tangazo la Serikali Namba 257 alichokinukuu kilishafanyiwa marejeo mwaka 2015 na kutangazwa katika Gazeti la Serikali mnamo tarehe 30/01/2015 na kuwa Kanuni namba 30/2015 ya Sheria ya Usalama Barabarani ambayo imelenga kutengeneza mfumo wa ulipaji wa tozo za papo kwa papo kwa njia ya kielektroniki. Kanuni hii pia inasomwa pamoja na Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168 iliyorejewa mwaka 2002, kifungu cha 95.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukamataji wa magari na kisha kuyashikilia upo kisheria, kifungu cha 87, kifungu kidogo cha (a), (b) (c) na (d) cha Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168 iliyorejewa mwaka 2002, magari haya hushikiliwa kulingana na uzito wa kosa alilofanya dereva mfano makosa hatarishi kama ubovu wa gari ambapo gari linatakiwa likafanyiwe ukaguzi na Mkaguzi wa Magari, makosa ambayo dereva au mmiliki anatakiwa apelekwe Mahakamani na kadhalika.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa ulipaji tozo za papo kwa papo kwa njia ya mtandao ulianza kutekelezwa kwa majaribio katika Mikoa mitatu ya Kipolisi ya Ilala, Kinondoni na Temeke ambapo jumla ya mashine za kielektroniki (POS) 360 na kamera za kufuatilia magari yanayodaiwa faini (ANPR) 3 zilizotumika na kuonyesha ufanisi na mafanikio makubwa. Kuanzia Apili, 2018, mfumo huu ulianza kutumika nchini kote ambapo mashine hizi za kielekroniki (POS) zipatazo 3,000 zilipelekwa mikoa yote nchini na mashine za ufuatiliaji wa magari (ANPR) zipatazo 400 zinatarajia kusambazwa mikoa yote nchini kuondoa usumbufu usio wa lazima.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani juu ya raia wa kigeni wanaopewa vibali vya kuja kufanya kazi hapa nchini kwa muda na kuwazalisha watoto na wadogo zetu na inapofika muda wa kuondoka huwakimbia na kuwaacha watoto hao wakiishi maisha yao yote bila baba kitu ambacho huwasababishia unyonge katika maisha yao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Magharibi, kama Ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Uhamiaji inatoa vibali vya ukaazi nchi kwa wageni baada ya Wizara ya Kazi kutoa vibali vya kazi kwa wageni hao.

Mheshimiwa Spika, mikakati ambayo Serikali inachukua ni kuelimisha raia wa Tanzania kuwa wasidhani kila mgeni anayekuja kufanya kazi Tanzania ni mtu mwema au ana uwezo wa kifedha na kutegemea kuwa atasaidiwa na mtoto wake kwenye malezi, hivyo kuwa waangalifu ili kuepuka madhara yanayoweza kutokea kutokana na kujiingiza kwao katika mahusiano ya kimapenzi na watu wasiowafahamu vema ikiwemo mimba na maradhi yanayosababishwa na ngono.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Gereza katika Wilaya ya Chunya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hadi sasa nchini kuna Wilaya 51 ambazo hazina Magereza ya Wilaya ikiwemo ya Chunya. Hata hivyo, lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa kila Wilaya inakuwa na Gereza ili kuwahifadhi wahalifu wa Wilaya husika, kwani uwepo wa Gereza kwenye kila Wilaya utapunguza gharama za kuwasafirisha wahalifu kutoka Wilaya moja na kuharakisha uendeshwaji kesi sambamba na kupunguza msongamano wa mahabusu.

Mheshimiwa Spika, hadi sasa Serikali inaendelea na mpango wa ujenzi wa magereza kwa awamu kwenye Wilaya zisizokuwa na magereza. Hata hivyo, kasi ya ujenzi huo imekuwa ni ndogo kutokana na kuathiriwa na uhaba wa rasilimali fedha. Hivyo Serikali inadhamiria kujenga na kuendelea na ujenzi huo kwenye Wilaya zisizo na Magereza ikiwemo Wilaya ya Chunya kadri ya hali ya Bajeti itakavyoruhusu.
MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:-

Imekuwa ni kawaida sasa kwa Askari wa Usalama barabarani kusimamisha magari ya usafiri wa Umma kama vile daladala na mabasi na kadhalika:-

Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kuwa na Vituo Maalum vya Ukaguzi huo ili kuokoa muda wa wasafiri?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rose Cyprian Tweve, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Usalama Barabani, Sura ya 168 iliyorejewa mwaka 2002 Kifungu cha 81, kinampa uwezo Askari Polisi wa kulisimamisha gari lolote barabarani au sehemu yoyote anapolitilia shaka na kulikagua au pindi linapokuwa limetenda kosa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani limeshaandaa utaratibu wa kuwa na vituo maalum vya ukaguzi wa mabasi ya Umma katika vituo vikuu vya mabasi vyote katika kila Mkoa ambapo mabasi ya abiria hufanyiwa ukaguzi kabla ya kuanza safari na pale yanapofika mwishoni wa safari.

Mheshimiwa Spika, aidha, ukaguzi wa pembezoni mwa barabara (road side inspection) ambao huhusisha mabasi ya daladala na vyombo vingine vya moto hufanyika katika vituo vya ukaguzi maalum (check points) ambavyo vipo katika barabara kuu na katika barabara nyingine za Miji pamoja na Majiji.
MHE. MATTAR ALI SALUM aliuliza:-

Jeshi la Polisi lipo kwa mujibu wa sheria na hupaswa kufanya kazi kwa mujibu wa sheria za nchi. Jeshi la Polisi linapowakamata baadhi ya watu huamuru wawekwe ndani zaidi ya saa 24 na kusababisha usumbufu mkubwa:-

Je, ni kesi zipi mtuhumiwa anapaswa kuwekwa ndani chini ya saa 24.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mattar Ali Salum, Mbunge wa Shaurimoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, makosa yote isipokuwa yaliyoainishwa katika kifungu 148(5)(a)-(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20 yana dhamana. Watuhumiwa wake hawapaswi kukaa mahabusu zaidi ya saa 24. Aidha, watuhumiwa ambao wanakaa ndani zaidi ya saa 24 ilhali makosa yao yana dhamana hutokana na sababu kwamba watuhumiwa hao wameshindwa kutimiza masharti na vigezo vya kupata dhamana kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa la Jinai Kifungu cha 65 na 66, Sura ya 20 kama ambavyo imefanyiwa mapitio mwaka 2002.
MHE. MACHANO OTHMAN SAID aliuliza:-

(a) Je, ni Wizara ipi inayo wajibika kukusanya fedha za Viza na kusimamia utoaji wa Viza hizo?

(b) Je, kuna mgao wowote kwenda Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia uwanja wake wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Karume?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Machano Othman Said, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi lenye sehemu (a) na (b) yote kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Uhamiaji ndiyo inayowajibika kukusanya fedha za Viza na kusimamia utoaji wa Viza. Aidha, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Balozi za Tanzania ndiyo inayo kusanya fedha za Viza na kusimamia utoaji wa Viza katika Balozi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makusanyo yote ambayo yanayokusanywa na Idara ya Uhamiaji Zanzibar kupitia vyanzo vya mapato ikiwemo mapato yatokanayo na Viza kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume huwasilishwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:-

Vitendo vya utekaji kwa watu wasio na hatia na kuwatesa, kuwahujumu na hata kuwaua vinaendelea kukithiri nchini:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzuia, kulinda na kuhakikisha inakomesha vitendo hivyo haraka sana?

(b) Je, hadi sasa ni watu wangapi ambao wamekamatwa na kuchukuliwa hatua kutokana na uhalifu huo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mbunge wa Wingwi, lenye Sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, jukumu la msingi la Serikali ni kuhakikisha raia wake wanakuwa salama wakati wote na wanaendelea na shughuli za uzalishaji mali na shughuli nyingine za kijamii kwa amani na utulivu pasipokuwa na hofu. Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kwenye taarifa za utekaji, utesaji ama mauaji zinapotolewa lengo likiwa ni kuwabaini, kuwachukulia hatua za kisheria watu ambao wanajihusisha na vitendo hivyo.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutumia taarifa za kiitelijensia imekuwa ikiweka mikakati mbalimbali ya kudhibiti mipango ya wahalifu kwa kufanya operesheni na doria mbalimbali kwa lengo la kuzuia na kukomesha vitendo vya aina hii ambapo hadi sasa mtuhumiwa mmoja amekamatwa kwa makosa ya utekaji nyara.
MHE. MACHANO OTHMAN SAID (K.n.y. MHE. BAGWANJI MAGANLAL MEISURIA) aliuliza:-

Mara nyingi wakati wa chaguzi mbalimbali Zanzibar kunatokea hali ya fujo na ukosefu wa amani na kusababisha wananchi kukosa amani na wakati mwingine kutoshiriki katika chaguzi husika:-

Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Zanzibar juu ya suala hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maganlal Meisuria, Mbunge wa Chwaka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa nyakati za uchaguzi hukumbwa na vitendo vya uvunjifu wa amani hususani wakati wa kampeni na wakati wa kupiga kura. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi huchukua hatua mbalimbali kudhibiti vitendo hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napenda kuwafahamisha wananchi kuwa ni jukumu la Serikali kuhakikisha amani na utulivu vinatamalaki nchini wakati wote bila kujali nyakati au majira mbalimbali katika mwaka. Jeshi la Polisi linaendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa Askari ya ukakamavu, upelelezi na kuongeza vitendea kazi ili kuwajengea uwezo na weledi wa kuzuia na kukabiliana na vitendo vya uvunjifu wa amani vinavyojitokeza hususani wakati wa uchaguzi.
MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-

Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi katika mazingira magumu sana kutokana na uchakavu wa vitendea kazi pamoja na kukosekana kwa magari ya kutosha:-

(a) Je, ni lini Serikali itawapatia magari Askari Polisi wa Wilaya ya Masasi kutokana na kutokuwa na magari ya kutosha?

(b) Je, ni lini Serikali itarekebisha utaratibu uliopo ambapo askari wanalazimika kutoa pesa zao za mfukoni kuwapa chakula mahabusu?

(c) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za askari katika Wilaya ya Masasi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uhaba wa vitendea kazi kwa Jeshi la Polisi ikiwa ni pamoja na uchache wa magari. Kwa sasa Wilaya ya Masasi imeshapatiwa gari moja aina ya Leyland Ashok, hivyo kufanya kuwepo kwa magari matatu ambayo ni PT 1865, Toyota Landcruiser, PT 4011 Grand Tiger na Leyland Ashok. Gari hili jipya litatumika kwa shughuli mbalimbali kama doria na operesheni kubwa. Aidha, kutokana na jiografia ya Wilaya ya Masasi, Jeshi la Polisi litaiongezea Wilaya ya Masasi magari kwa kadri yatakavyopatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna utaratibu waAskari Polisi kutoa pesa zao mfukoni kwa ajili ya chakula cha mahabusu, bali utaratibu uliopo ni kwamba Serikali kupitia Jeshi la Polisi lina wajibu wa kuwapatia chakula mahabusu waliopokorokoroni ingawa pia ndugu za mahabusu wanaruhusiwa kuwapelekea chakula jamaa zao walioko korokoroni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Masasi ina nyumba za makazi ya askari zipatazo 15 ambazo zinaishi familia za askari 30, ingawa ni kweli askari wengine wapatao 154 bado wanaishi uraiani. Hata hivyo, Serikali itaendelea kujenga nyumba za makazi ya Askari kwa awamu kwa kadri upatikanaji wa fedha utakavyoruhusu.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA (K.n.y. MHE. ISSA A. MANGUNGU) aliuliza:-

Serikali ilianzisha Kanda Maalum ya Kipolisi Dar es Salaam na kufanya Wilaya ya Temeke kuwa Mkoa wa Kipolisi; tangu Temeke iwe Mkoa wa Kipolisi kumekuwa na ongezeko kubwa la uhalifu hasa maeneo ya Jimbo la Mbagala:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kituo cha Mkuu wa Polisi Wilaya ya Mbala?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Vituo vya Polisi na kuviongezea askari, vitendea kazi na kujenga nyumba za askari katika maeneo ya Jimbo la Mbagala?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mbagala ni Wilaya mpya ya Kipolisi iliyopo katika Mkoa wa Kipolisi wa Temeke. Kama ilivyo kwa wilaya nyingine katika Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Wilaya ya Mbagala inahitaji kujengewa Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Wilaya. Kwa sasa wananchi wa Mbagala wanahudumiwa katika Kituo cha Polisi cha Mbagala Kizuiani ambacho miundombinu yake haitoshelezi. Aidha, hali kibajeti itakaporuhusu, Serikali itaweka mpango wa kuwajengea wananchi wa Mbagala Kituo kipya cha Polisi, nyumba za makazi ya askari na ofisi ya Mkuu wa Polisi wa Mbagala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza kukabiliana na uhalifu, Wilaya ya Kipolisi Mbagala imepata mgao wa magari matatu (3) aina ya Leyland Ashock Stile yenye Na. PT 3779; PT 3881 na PT 3891 na kufanya jumla ya magari yote katika Wilaya ya Mbagala kuwa tisa ambayo yanatumika kwa shughuli za doria, upelelezi na operesheni mbalimbali kwa ajili ya kuimarisha usalama katika Wilaya ya Mbagala.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na baadhi ya Askari wa barabarani wanaosimamisha magari hasa yale ya safari ndefu wakitokea vichakani (kujificha) na hatimaye wakati mwingine kusababisha ajali:-

Je, ni Askari wangapi kama hawa wameshachukuliwa hatua za kinidhamu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi nchini chini ya Sheria ya Usalama Barabarani Sura 168 iliyorejewa mwaka 2002, inamtaka Askari wa Polisi kuhakikisha usalama wa watumiaji wote wa barabara. Katika kutekeleza hilo, Polisi wanatumia mbinu mbalimbali kwa mujibu wa sheria na taratibu ambazo zinawaongoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako Tukufu litakumbuka kuwa wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani kulikuwa na mfululizo wa ajali nyingi barabarani hususan zile ambazo zinahusisha magari ya abiria. Kwa kuzingatia hilo, Baraza la Usalama Barabarani lilibuni mkakati maalum uliofanikisha kupunguza ajali kwa asilimia 43 mpaka sasa. Mkakati huu ulihusisha mbinu mbalimbali zenye lengo la kuwalazimisha madereva kufuata sheria za usalama barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina ushahidi wa matukio ya askari waliowahi kusababisha ajali barabarani kwa sababu ya kujificha. Hata hivyo, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Usalama Barabarani limejiwekea utaratibu wa kufanya uchunguzi wa kina kwa kila ajali kubwa inayotokea na kuchukua hatua stahiki inapobainika kuna uzembe wa usimamizi wa sheria au uvunjifu wa Sheria za Usalama Barabarani.
MHE. MOHAMMED JUMA KHATIB aliuliza:-

Je, ni katika mazingira gani Askari Polisi anapaswa au hulazimika kumtesa Mtuhumiwa wa makosa mbalimbali wakati akiwa mikononi mwake au kwenye Kituo cha Polisi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohammed Juma Khatibu, Mbunge wa Chonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20, kifungu cha 11 kinaelekeza namna ya ukamataji. Aidha, kifungu hiki mahsusi cha ukamataji, hakimruhusu askari kumpiga au kumtesa mtuhumiwa wa makosa mbalimbali wakati akiwa mikononi mwa Polisi au kwenye Kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Spika, Kanuni za Kudumu za Utendaji wa Jeshi Polisi la (PGO) zinakataza na kuelekeza utendaji mzuri wa Askari Polisi, ambapo askari yeyote atakapobainika kufanya vitendo vya kumpiga au kumtesa mtuhumiwa huchukuliwa hatua za kunidhamu ikiwepo kufukuzwa kazi na au kufikishwa Mahakamani.
MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-

Kumekuwa na ajali za barabarani za kutisha katika Milima ya Sukamahela eneo la Mbwasa, Manyoni na Sekenke Shelui:-

(a) Je kwa kipindi cha miaka miwili yaani 2016 na 2017, ni ajali ngapi zimetokea katika milima tajwa?

(b) Je, ni watu wangapi wamepoteza maisha na wangapi walijeruhiwa katika kipindi hicho?

(c) Je, Serikali inatoa tamko gani ili kupunguza au kukomesha kabisa ajali katika maeneo haya ndani ya Mkoa wa Singida?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Manyoni Mashariki, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya ajali 28 zimetokea katika kipindi cha miaka miwili yaani tarehe 1 Januari, 2016 mpaka tarehe 31 Disemba, 2017 katika sehemu hiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya watu 33 wamepoteza maisha na jumla ya watu 26 walijeruhiwa katika kipindi tajwa.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inawataka madereva kuwa makini wanapoendesha vyombo vya moto barabarani na wazingatie sharia, kanuni, taratibu na alama na michoro ya barabarani. Pia waendeshe kwa kuzingatia udereva wa kujihami (defensive driving) ili kuepusha ajali, kwani ajali nyingi zinazotokea katika maeneo haya zinasababishwa na uzembe wa madereva, ubovu wa magari, uchovu wa madereva hususani kwenye uwepo wa kona kali, milima na miteremko mikali.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-

Kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu ya malimbikizo ya madeni mbalimbali ya wazabuni wanaotoa huduma mbalimbali ikiwepo huduma ya kupeleka chakula kwa wanafunzi magerezani na matengenezo ya magari.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kulipa madeni hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika nyakati tofauti imekuwa na mkakati wa kulipa madeni yake ya ndani ikiwemo madeni ya watoa huduma, chakula cha wafungwa na matengenezo ya magari katika magereza yote nchini.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 hadi mwaka wa fedha 2018/2019 jumla ya kiasi cha fedha shilingi 23,563,630,710.61 zimelipwa kwa ajili ya watoa huduma za uendeshaji, chakula cha wafungwa na matengenezo ya magari yakiwa ni madeni ya mwaka wa fedha 2014/2015 hadi 2016/2017.

Mheshimiwa Spika, madeni ya mwaka 2012/2013 mpaka mwaka 2013/2014 na 2017/2018 tayari yameshahakikiwa, kinachosubiriwa ni fedha kutoka Hazina kwa ajili ya kulipa. Hata hivyo, madeni ya mwaka wa fedha 2018/2019 tayari yameandaliwa yanasubiri uhakiki kutoka Hazina ili kuhakiki madeni hayo na baadaye kuyalipa.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kulipa madeni ya wazabuni wanaotoa huduma mbalimbali ikiwemo chakula cha wafungwa na matengenezo ya magari kadri ya fedha itakavyopatikana.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati gereza la Keko ambalo miundo mbinu yake imechakaa sana?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Ally Mtolea, Mbunge Wa Temeke, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Gereza la Keko ni moja ya magereza yaliyojengwa wakati wa mkoloni, hivyo hata miundombinu yake imekuwa ni ya muda mrefu inayohitaji ukarabati. Hata hivyo, Serikali imekuwa ikifanya jitahada za ukarabati kulingana na fedha inavyopatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali ilifanya ukarabati wa mfumo wa maji taka kwa kuchimba mashimo ya kuhifadhia majitaka baada ya mashimo yaliyokuwepo kuzidiwa kutokana na idadi kubwa ya wahalifu waliomo ndani ya gereza hilo.
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI aliuliza:-

Wapo akina mama wanaojifungua wakiwa gerezani na kuendelea kutumikia adhabu zao huku wakiwa na watoto wachanga:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapumzisha kama miezi sita bila kufanya kazi ili wapate nguvu kwanza?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alfredina Apolinary Kahigi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wapo wafungwa wanawake wanaoingia na ujauzito gerezani na kujifungua wakiwa bado wanatumikia adhabu zao. Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Jeshi la Magereza inatambua umuhimu wa kumpatia huduma stahiki pamoja na kutofanya kazi ngumu kwa mama mjamzito na aliyejifungua akiwa gerezani, ili aweze kumnyonyesha na kumhudumia mwanae inavyostahili mfano, kupelekwa kliniki, kupewa maziwa kwa ajili ya mwanae, chakula cha ziada na kutengwa na wenzie kwa kipindi kisichopungua miezi mitatu ili aweze kujihudumia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za wafungwa hawa zimeainishwa vizuri katika Kanuni za Kudumu za Uendeshaji wa Jeshi la Magereza kifungu Na. 728 - 729 Toleo Na. 4 la mwaka 2003.
MHE. SABREENA H. SUNGURA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza mahabusu katika Magereza na Vituo vya Polisi nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Hamza Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi hiki kirefu Serikali kupitia vyombo vyake vya haki jinai nchini imekuwa ikifanya juhudi mahususi kupunguza idadi ya mahabusu katika Magereza yote hapa nchini. Kupitia mikakati mbalimbali idadi ya mahabusu imekuwa ikipungua mara kwa mara na bado juhudi zinaendelea za kuhakikisha Magereza yetu yanahifadhi wahalifu kulingana na uwezo wake kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mikakati inayotumika kutatua tatizo la mahabusu Magerezani ni pamoja na Vikao vya Kamati za Kusukuma Kesi (Case Flow Management Committee), Idara ya Mahakama kusisitiza matumizi ya Sheria ya Dhamana kwa makosa yanayodhaminika, uundwaji wa kikosi kazi cha haki jinai kupitia makosa mbalimbali (Criminal Justice System Task Force) pamoja na mikakati mingine inayotokana na Idara ya Mahakama.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-

Je, Serikali inahakikishaje amani na utulivu vinakuwepo katika chaguzi mbalimbali nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwafahamisha wananchi kuwa ni jukumu la Serikali kuhakikisha kuwa amani na utulivu vinatamalaki nchini wakati wote bila kujali nyakati au majira mbalimbali katika mwaka. Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama limejipanga vizuri kudhibiti vitendo mbalimbali vya uvunjaji wa sheria ikiwemo fujo au aina yeyote ya ukosefu wa amani vinavyoweza kusababisha wananchi kushindwa kushiriki katika shughuli zao za kila siku, ikiwemo kushiriki katika michakato ya chaguzi mbalimbali zinazofanyika nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inaendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa askari wake wa ukakamavu, upelelezi na kuongeza vifaa vya kutenda kazi ili kuwajengea uwezo na weledi mkubwa wa kuweza kuzuia na kukabiliana na vitendo kama hivyo vinavyojitokeza nyakati za uchaguzi.
MHE. JOHN W. HECHE (K.n.y MHE. KABWE Z. R. ZITTO) aliuliza:-

Watanzania wanaoishi nje ya nchi wanapata changamoto za huduma za uhamiaji kutokana na Balozi zetu takribani zote kutokuwa na Maafisa Uhamiaji.

Je, ni lini Serikali itapeleka Maafisa Uhamiaji kuhudumu kwenye Balozi zetu ili kutoa huduma bora kwa raia wa Tanzania kwenye nchi hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI, alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zitto Kabwe Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Uhamiaji inawajibika kuhakikisha Watanzania wanaoishi nje ya nchi wanapata huduma bora za uhamiaji wanapofika kwenye Balozi zetu nje ya nchi. Maafisa Uhamiaji waliokuwa wanatoa huduma za uhamiaji katika Balozi zetu ama wamestaafu au wamemaliza muda wao wa kuhudumu katika Balozi walizokuwa na wamerejea nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha huduma bora za uhamiaji zinaendelea kutolewa kwa raia wa Tanzania wanaoishi nje ya nchi, tayari Serikali imewateua maafisa watano kutoka Idara ya uhamiaji ambao wamepatiwa mafunzo ya kuhudumu katika Balozi. Kwa sasa Idara ya Uhamiaji kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wako katika hatua za mwisho za kukamilisha taratibu za kuwapeleka Maafisa hao kwenda kuhudumu katika Balozi walizopangiwa.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya watoto wachanga kutupwa majalalani, mitaroni na katika mifuko ya rambo:-

(a) Je, nini kauli ya Serikali kuhusu matukio hayo?

(b) Je, ni watuhumiwa wangapi walishakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vitendo vya kutupa watoto majalalani, mitaroni na maeneo mengine ni kinyume na sheria za nchi na haki za binadamu. Kwa mujibu wa Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 chini ya kifungu cha 218 na 219, adhabu ya makosa hayo ni kifungo cha maisha. Aidha, Serikali inalaani vikali vitendo hivyo na itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya wale watakaopatikana na hatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu za matukio ya kutupa watoto wachanga zinaonesha kuwa katika kipindi cha mwezi Januari hadi Juni, 2019 kumekuwa na jumla ya matukio 66 ya watoto waliopatikana wakiwa wametupwa, 43 kati yao waliokutwa hai na 23 walikutwa wamefariki. Aidha, watuhumiwa 18 walikamatwa na kufikishwa mahakamani na kesi zao zipo katika hatua mbalimbali.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO (K.n.y. MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS) aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kufunga Kamera ndani ya Vituo vya Polisi sasa ili kupunguza malalamiko kwa baadhi ya wananchi wanapohudumiwa kwa kumwezesha Mkuu wa Kituo kufuatilia mwenendo wa shughuli za Kituo akiwa Ofisini au kwa kutunza kumbukumbu za matukio yanayotokea kwenye vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la matumizi ya CCTV Camera katika vituo vyetu ni la umuhimu mkubwa katika kuhakikisha huduma ya Polisi kwa wananchi zinatolewa kwa weledi na kwa kuzingatia maadili ya Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi lina nia ya kufanya maboresho yakiwemo matumizi ya TEHAMA kwa kufunga kamera katika vituo vyake ili kuwapa nafasi Viongozi wa Kamandi kufuatilia matukio mbalimbali yanayotokea vituoni ikiwemo namna Askari wa chini wanavyohudumia wananchi.

Aidha, kutokana na ufinyu wa bajeti unaochangiwa na wingi wa changamoto, Jeshi la Polisi kwa sasa halina bajeti hiyo. Hata hivyo, limeruhusu wadau katika maeneo mbalimbali kuwezesha ufungaji wa kamera za ufuatiliaji kwa nia ya kuboresha na kufuatilia utendaji wa Askari.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kushirikisha wadau katika maeneo yao kuchangia upatikanaji na ufungaji wa CCTV Camera vituoni ili kupunguza malalamiko ya huduma isiyo na weledi ya Askari kwa wananchi.
MHE. WILLIAM D. NKURUA aliuliza:-

Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Nanyumbu kinatumia majengo ya nyumba za kuishi Askari Polisi:-

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Nanyumbu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa William Dua Nkurua, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Nanyumbu ni miongoni mwa wilaya mpya ambayo ilianzishwa mwaka 2007 hivyo baada ya mabadiliko haya ililazimu jengo ambalo lilikuwa likitumika kama Kituo kidogo cha Polisi kata kuanza kutumika kama Kituo cha Polisi Wilaya.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inatambua changamoto za ukosefu wa vituo vya polisi na ofisi katika wilaya mpya zilizoanzishwa hivi karibuni ikiwemo Wilaya ya Nanyumbu. Jitihada zinaendelea kufanyika za ujenzi wa vituo vya polisi na ofisi za wakuu wa polisi wa wilaya hizo kadiri fedha kutoka kwenye bajeti ya maendeleo na vyanzo vingine vinavyopatikana.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-

Ni kosa la Jinai kwa Mtu au Vyombo vya Habari kutoa, kuandika, kusambaza au kutangaza habari za uongo. Je, Jeshi la Polisi linachukua hatua gani stahiki kwa watu au vyombo vya habari vinavyofanya makosa hayo?
NAIBU WAZIRI YA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatibu Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linao utaratibu unaotumika pindi mtu anapokuwa ametenda makosa ya jinai ambapo ushahidi hukusanywa kisha jalada huandaliwa kwenda kwa Mwanasheria wa Serikali; na ushahidi ukijitosheleza, mtuhumiwa hufikishwa Mahakamani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mamlaka kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari Na. 12 ya Mwaka 2016 ambapo inaelekeza kuchukua hatua kwa chombo cha habari kilichotoa taarifa za uongo ikiwa ni pamoja na kufuta leseni au kusimamisha leseni kwa muda pale ambapo chombo cha habari kimekiuka masharti ya leseni hiyo.
MHE. NEEMA W. MGAYA (K.n.y. MHE. DEO K. SANGA) aliuliza:-

Askari wa Kituo cha Polisi katika Mji wa Makambako hawana gari la doria wala nyumba za kuishi:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za kuishi Askari hao?

(b) Je, ni lini Serikali itatoa gari la doria kwa Kituo cha Polisi Makambako?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Makambako ina askari wapatao 111 na kuna jumla ya nyumba 12 tu katika Mji wa Makambako. Nyumba hizo ni takribani asilimia 11 ya mahitaji halisi ya nyumba za makazi na askari katika mji huo. Hata hivyo, katika jitahada za kutatua changamoto hiyo, mwezi Oktoba, 2018 Serikali imeanzisha ujenzi wa nyumba 20 katika Mji wa Makambako ambapo nyumba hizi kwa sasa zimeshakamilika na askari wameshahamia.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Makambako kwa sasa ina magari matatu; magari mawili ya zamani ambapo moja ni PT. 0766 Landrover inayohitaji matengezo makubwa ili liweze kufanya kazi; na nyingine ni aina ya PT.1912 Toyota Land Cruiser ambayo ndiyo inatumika ingawa inafanyiwa matengenezo ya hapa na pale. Gari hili ndiyo inalotumika kwenye doria na operesheni mbalimbali pamoja na kupeleka askari kwenye matukio makubwa yanayotokea sehemu za mbali. Doria katika Mji wa Makambako hufanyika kwa kutumia gari, miguu pamoja pikipiki.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, mwezi Septemba mwaka 2018 Wilaya ya Makambako imepata mgao wa gari jipya moja aina ya Ashok Leyland kwa ajili ya kusaidia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Jeshi la Polisi katika wilaya hiyo. (Makofi)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-

Majanga ya moto yamekuwa yakitokea mara kwa mara hasa Viwandani, Majumbani na katika majengo ya Serikali:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa mafunzo kwa Wafanyakazi na wananchi juu ya mbinu za kujihami na kujiokoa katika majanga ya moto?

(b) Je, Serikali imejipangaje katika kutoa mafunzo katika maeneo ya kazi na wananchi juu ya matumizi ya mitungi ya kuzima moto (Fire Extinguishers)?

(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kukagua mitungi hiyo kama bado inafaa kwa matumizi au imeshapita muda wake wa kutumika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kaskazini Unguja, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea kutoa mafunzo ya mbinu za kujihami na jinsi ya kujiokoa katika majanga ya moto kwenye maeneo ya kazi na wananchi kwa ujumla. Elimu dhidi ya kinga na tahadhari ya moto imeendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo maeneo yenye mikusanyiko ya watu kama vile masoko, Shule za Sekondari na Msingi, Vyuo, Makanisani na Misikitini kupitia vyombo mbalimbali vya habari vikiwemo magazeti, radio na televisheni.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limejipanga vyema kutoa mafunzo kwenye maeneo ya kazi na wananchi juu ya matumizi ya mitungi ya kuzimia moto kwa kuanzisha kampeni mbalimbali kama vile “Ninacho, Ninajua Kukitumia,” “Mlango kwa Mlango” na “Nyumba Salama” zenye lengo la kuhamasisha watu kuwa na vizimia moto na kujua kuvitumia katika maeneo ya makazi, viwanda, maeneo ya vyombo vya usafiri na usafirishaji, majumbani, maeneo ya biashara na katika mikusanyiko mikubwa ya watu. Aidha, wananchi wanaendelea kupatiwa elimu na mafunzo juu ya mifumo yote ya kuzima kuzima katika majengo na maeneo mbalimbali ili kuepusha majanga ya moto.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Ukaguzi wa tahadhari na kinga dhidi ya moto kwa mujibu wa Kanuni za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji umeendelea kufanyika sambasamba na ukaguzi wa mitungi ya kuzima moto na kumshauri mtumiaji juu ya ubora wa mtungi na kumshauri mmiliki ipasavyo.
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza:-

Kijiji cha Sojo katika Kata ya Isugule, Wilayani Nzega patajengwa Kituo kikubwa (coating yard) cha kuandaa mabomba yote ya mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima, Uganda hadi Chongoleani, Tanga ambapo Kituo hicho kitakuwa na wafanyakazi zaidi ya 2,000; kutokana na ongezeko hilo la idadi ya watu mahitaji ya huduma za Jamii yatakuwa makubwa:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Kituo kidogo cha Polisi katika Kijiji cha Sojo ili kuhakikisha usalama kwa wananchi na mali zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi iliona umuhimu wa kuwepo kwa Kituo cha Polisi katika Kijiji cha Sonjo ambapo ndipo kitakapojengwa kituo cha kuandaa mabomba ya mafuta toka Uganda kuja Tanzania. Aidha, juhudi mbalimbali zimekwishaanza ambapo Uongozi wa Polisi Mkoa wa Tabora kwa kushirikiana na Uongozi wa Halmashauri ya Mji wa Nzega wanaendelea na utaratibu wa kupata eneo la kujenga Kituo cha Polisi kitakachokuwa na hadhi ya daraja ‘C’ ambacho kitakuwa na Askari kuanzia kumi na tano (15), pia eneo la ujenzi wa nyumba za kuishi askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa wananchi wa Sonjo wanapata huduma ya Polisi katika Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Nzega.
MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-

Matukio ya watu kupoteza maisha kutokana na ajali za moto yamezidi kuongezeka nchini:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukiwezesha Kikosi cha Zimamoto ili kufanya kazi ipasavyo kwenye Miji na nje ya Miji?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuimarisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili liweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Pia, Serikali imekuwa ikitenga na itaendelea kutenga fedha za maendeleo katika bajeti ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kila mwaka kwa ajili ya ununuzi wa magari ya kuzima moto pamoja na vifaa mbalimbali vya kuzima moto na uokoaji ili kutoa huduma zake ipasavyo ikiwemo kwenye miji na nje ya miji.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji inashirikiana na Shirika la Nyumbu katika utengenezaji wa magari mapya ya kuzima moto na uokoaji. Pia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limesaini hati ya makubaliano na Kampuni ya ROM Solution ili kupata mkopo wenye masharti nafuu utakaowezesha kupata vitendea kazi mbalimbali ikiwemo magari ya kuzimia moto na uokoaji pamoja na vifaa nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo nje ya Miji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea kutoa elimu kwa Umma ya kuzuia na kupambana na majanga mbalimbali ili kuzuia na kupunguza matukio ya moto nchini. Pia, Serikali inaendelea kuwasisitiza wananchi kumiliki vizimia moto katika maeneo yao ili kuukabili moto katika hatua za awali.
MHE. ASHA ABDULLA JUMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mfumo gani wa kupandishwa daraja askari wenye vyeo vya chini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika,kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdulla Juma, Mbunge wa Viti Maalumkama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika,Vyombo vya Usalama vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi vina mfumo wa Upandishwaji wa madaraja kwa askari wa vyeo vya chini ambayo huzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo umbele kwa maana ya seniority, miaka mitatu ya cheo alichonacho, tabia njema, nidhamu, utendaji mzuri, umahiri wa kazi, elimu au utaalamu mahsusi, uwezo wa kumudu madaraka ya cheo anachopandishwa, kutokuwa na tuhuma zinazochunguzwa wala mashtaka ya Kijeshi katika kipindi cha miaka mitatu na bajeti tengefu kwa mwaka husika.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. HASNA S. K. MWILIMA) aliuliza:-

Wilaya ya Uvinza imeanzishwa tangu mwaka 2002 lakini hadi sasa Jeshi la Polisi katika Wilaya hii halina nyumba za kuishi, Ofisi pamoja na vitendea kazi:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha vitendea kazi Jeshi la Polisi katika Wilaya hiyo kama vile magari, Ofisi pamoja na makazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Mwilima, Mbunge Wa Kigoma Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi lina jumla ya Wilaya 168 za kipolisi ikiwa ni pamoja na Wilaya za Kiserikali. Kati ya hizo Wilaya 127 zina majengo kwa ajili ya Ofisi na Vituo vya Polisi vya Wilaya ikiwemo Wilaya ya Uvinza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali kuliboresha Jeshi la Polisi kwa awamu. Mathalani, Serikali imejenga na inaendelea kujenga nyumba za makazi kwa askari nchi nzima katika ngazi ya Mkoa na ni mpango wa Serikali kujenga Ofisi na nyumba za kuishi askari katika ngazi za wilaya zote nchini. Aidha, Wilaya ya Uvinza ina magari mawili ambayo ni T/Land cruiser PT 1415 linalotumiwa na OCD na Leyland Ashock kwa matumizi mbalimbali ya Kipolisi.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA) aliuliza:-

Waendesha pikipiki (bodaboda) nchini wamekuwa wakikamatwa na Askari wa Usalama Barabarani mara kwa mara kwa tuhuma za makosa mbalimbali:-

Je, zoezi hili la ukamataji wa waendesha pikipiki limefanikiwa kwa kiasi gani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja ya chanzo cha ajali za barabarani huchangiwa na waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda. Mathalan mwaka 2016 nchini kote kulitokea jumla ya ajali za pikipiki 2,544 zilizosababisha vifo vya watu 890 na majeruhi 2,128. Mwaka 2017 zilitokea ajali za pikipiki 1,459 zilizosababisha vifo vya watu 728 na majeruhi 1,090. Mwaka 2018 zilitokea ajali za pikipiki 876 ambazo zilisababisha vifo vya watu 366 na majeruhi 694.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Januari hadi Juni, 2019 kumetokea ajali za pikipiki 334 zilizosababisha vifo 176 na majeruhi 289. Ukilinganisha na kipindi kama hicho cha Januari hadi Juni, 2018 ambapo ajali zilitokea 408 zikasababisha vifo 165 na majeruhi 344, utaona kuwa ajali za pikipiki zimepungua sawa na asilimia 18 ingawa vifo viliongezeka kwa idadi ya 11 ambayo ni sawa na asilimia 6.6 na majeruhi kupungua kwa idadi ya 55 ambayo ni sawa na asilimia 16. Kwa ujumla takwimu hizi zinathibitsha kupungua kwa ajali za bodaboda barabarani ambazo zinatokana na waendesha pikipiki kutozingatia sheria.

Mheshimiwa Spika, kupungua kwa ajilia hizi ni mafanikio yanayopatikana kutokana na usimamizi wa Sheria za Usalama Barabarani kwa kuwachukulia hatua waendesha bodaboda ambao wanakiuka sheria na kuwachukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha Mahakamani.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-

Askari wa Jeshi la Polisi Zanzibar (Ziwani) wanakabiliwa na matatizo makubwa ya makazi kama vile miundombinu ya maji, nyumba chakavu, uhaba wa vyoo na kuharibika kwa uzio uliokuwepo katika eneo hilo unaohatarisha usalama wao:-

(a) Je, kuna mpango gani wa kufanyia matengenezo nyumba na vyoo kwa wakati huu?

(b) Je, Uzio wa boma hilo la Ziwani utafanyiwa ukarabati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi linakabiliwa na tatizo la uchakavu wa miundombinu kama majengo ya ofisi na nyumba za kuishi Askari kutokana na kuwa ya muda mrefu. Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikifanya ukarabati wa miundombinu hiyo kwa awamu ili kuboresha huduma kwa wananchi Mheshimiwa Spika Mipango ya ukarabati ya miundombinu hiyo kwa awamu ili kuboresha huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, mipango ya ukarabati wa miundombinu katika Kambi hiyo imeanza kwa kuandaa makadirio ya ukarabati kwa kuzingatia vipaumbele hasa kwa nyumba ambazo zimechakaa na ambazo zinaweza kukarabatika, mahitaji na gharama za majengo husika.

Mheshimiwa Spika, uzio wa Kambi ya Polisi - Ziwani ni wa fensi ya waya ambayo imezunguka eneo kubwa na waya huu katika baadhi ya maeneo ambao umechoka na kuchakaa kabisa. Aidha, upo mpango wa kujenga fensi ya matofali mara tu pale fedha zitakapokuwa zimepatikana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA (K.n.y. MHE. PETER A. LIJUALIKALI) Aliuliza:-

Jeshi la Magereza lilikuwa na mpango wa ujenzi wa Gereza Kitongoji cha Nakato na Kijiji cha Kibaoni, Wilaya ya Kilombero.

Je, mpango huu umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Peter Ambrose Lijualikali, Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kilombero ni miongoni mwa Wilaya 51 nchini ambazo hazina magereza. Mpango wa kuwa na magereza katika kila Wilaya una lengo la kupunguza tatizo la msongamano kwenye baadhi ya magereza yanayopokea wahalifu kutoka Wilaya zisizokuwa na magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kuwa na magereza kila Wilaya utarahisisha usikilizwaji wa kesi, wafungwa na mahabusu wataweza kupata huduma kwa urahisi kutoka kwa mawakili wao na pia kupunguza gharama za usafiri kwa ndugu zao wanapowatembelea magerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Magareza ina mpango wa kujenga magereza kwa Wilaya ambazo hazina magereza nchini ikiwemo Wilaya ya Kilombero. Aidha, mpango huu utatekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA (K.n.y. MHE. NAJMA MURTAZA GIGA) aliuliza:-

Utaratibu wa kuweka pamoja watuhumiwa wenye makosa tofauti kama vile, wizi wa kuku, mazao, mauaji, ujambazi sugu na ubakaji ni utaratibu wa kawaida katika magereza na mahabusu zetu hapa nchini, hali kadhalika kwa wafungwa wenye rika tofauti:-

(a) Je, Serikali haioni kuwaweka pamoja wafungwa na watuhumiwa hao ni hali hatarishi kwa mustakabali wa maisha yao ya baadae?

(b) Je, Serikali haioni inapoteza nguvu kazi ya vijana wetu kwa kuwachanganya pamoja na wale wabakaji hususan vijana wa kuanzia umri wa miaka 18 hadi 30?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya jukumu la Jeshi la Magereza ni kuwapokea na kuwahifadhi magerezani wahalifu wa aina zote wanaoletwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi. Sanjari na jukumu hilo, Kanuni za Uendeshaji wa Magereza za mwaka 1967 (The Prisons Management Regulations) zinaelekeza kuwa uhifadhi wa wahalifu magerezani utafanyika kwa kuzingatia utenganisho kwa vigezo vya jinsia, umri, kosa na kifungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa katika baadhi ya magereza yetu nchini hususani magereza yenye mahabusu, suala la kuwatenganisha wahalifu kwa kuzingatia vigezo vya umri, kosa na kifungo limekuwa halizingatiwi kutokana na sababu ya msongamano wa mahabusu na uhaba wa mabweni na hivyo kupelekea mahabusu kuchanganywa na wafungwa. Hata hivyo, katika kukabiliana na hali hiyo, Serikali imeshachukua hatua mbalimbali ikiwemo kujenga magereza katika Wilaya zisizokuwa na magereza, kufanya upanuzi na kujenga mabweni kwenye magereza na kutoa elimu kwa wahalifu juu ya madhara hasi ya vitendo ya uhalifu katika jamii na kutojihusisha na vitendo hivyo katika maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda ilieleweke kwamba kitendo cha wahalifu wa aina mbalimbali kuwemo magerezani au kuchanganywa hakuhalalishi wao kuendelea na vitendo vyao vya uhalifu kwani zipo Sheria, Kanuni na Taratibu za Magereza ambazo zinakataza na zinatoa adhabu kwa mhalifu endapo atabainika kufanya vitendo hivyo akiwa gerezani. Mathalani Kanuni ya makosa Gerezani ya Mwaka 1967 (The Prison Offences Regulations).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni hii imeainisha makosa mbalimbali ambayo mhalifu hapaswi kuyafanya akiwa gerezani sanjari na hatua za kuchukua na adhabu endapo itabainika ametenda kinyume. Hivyo msingi wa kanuni hii ni kuwataka wahalifu watambue kuwa wanapaswa wajirekebishe kwa kuachana na tabia ya kufanya vitendo vya kihalifu na pia Serikali inathamini na kulinda nguvu kazi yao.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA (K.n.y. MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS) aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua mgogoro wa muda mrefu kati ya kituo cha polisi Bububu na soko dogo la wananchi lililopo karibu na kituo hicho?

(b) Je, kiutaratibu umbali kati ya kituo cha polisi na makazi ya wananchi ni hatua ngapi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Galoss, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, si kweli kuwa kuna mgogoro wa kiwanja kati ya wananchi na Jeshi la Polisi katika eneo la kituo cha polisi Bububu. Ndiyo sababu wakazi wa eneo hilo ikiwemo wafanyabiashara wa soko hilo dogo hupata huduma za kiusalama katika kituo cha Bububu bila shaka yeyote. Aidha, kiwanja kilipojengwa kituo cha polisi Bububu na majengo mengine ya kituo yanamilikiwa kihalali na Jeshi la Polisi ingawa kuna kibanda cha kuuza samaki karibu na kituo hicho cha polisi kinachoitwa soko dogo la wananchi. Kibanda hicho kipo kati ya kituo cha Polisi Bububu na majengo mengine ya kituo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli upo utaratibu wa kuwepo kwa umbali kati vituo vya polisi, kambi za makazi ya askari ya wananchi. Hii ni kutokana na sababu za kiusalama kwa miundo mbinu ya Jeshi la Polisi. Aidha, kutokana na changamoto za makazi na ujenzi holela mijini. Uvamizi wa maeneo sehemu mbalimbali na kuongezeka kwa shughuli mbalimbali za kibinadamu zisizo rasmi imesababisha maeneo mengi ya vituo vya polisi kuingiliwa na kusogeleana na makazi ya wananchi.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:-

Pamoja na jitihada za vijana wengi kujiajiri wenyewe kwa kuendesha bodaboda wamekuwa wakisumbuliwa na polisi kwa pikipiki zao kukamatwa mara kwa mara:-

Je, kwa nini pikipiki zao zinapokamatwa na wanapoenda kuzichukua hukuta baadhi ya vifaa kama betri hazipo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Usalama Barabarani sura ya 168 iliyorejewa mwaka 2002 inampa mamlaka Askari Polisi kusimamisha chombo chochote barabarani na kukikagua kubaini kama kina makosa na hatimaye kukizuia na kukamata. Chombo cha moto kinapokamatwa hutunzwa kituoni kwa mujibu wa mwongozo wa Jeshi la Polisi Namba 229.

Mheshimiwa Spika, inapotokea kielelezo kimeharibiwa uchunguzi hufanyika na hatua kuchukuliwa kwa waliohusika na upotevu huo.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-

Tangu Wilaya ya Kilolo ipate hadhi ya kuwa wilaya mwaka 2002 Serikali haijaweza kujenga ofisi za polisi na nyumba za kuishi yalipo Makao Makuu ya Wilaya:-

Je, ni lini Serikali itajenga ofisi na nyumba hizo za polisi Wilaya ya Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabatti, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi lina jumla ya wilaya 168 za kipolisi na zile za Kiserikali, kati ya hizo 127 zina majengo kwa ajili Ofisi na vituo vya polisi na wilaya 41 zilizobaki hazina majengo kwa ajili ya ofisi na vituo vya polisi wilaya ikiwemo Wilaya ya Kilolo. Hii in atokana na ufinyu wa bajeti ya maendeleo kwa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Jeshi la Polisi limejikita kukamilisha miradi iliyokwisha anzishwa huko nyuma, pindi miradi hiyo itakapokuwa imekamilika na hali ya kibajeti itakapokuwa imeimarika Jeshi la Polisi litajikita katika ujenzi wa vituo vya polisi vya wilaya pamoja na nyumba za askari katika wilaya ambzo hazina majengo hayo ikiwemo Wilaya ya Kilolo.
MHE. MACHANO OTHMAN SAID aliuliza:-

Kwa muda mrefu kumekuwa na upungufu mkubwa wa Wafanyakazi wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar hali inayopunguza ufanisi wa kazi katika Idara hiyo?

(a) Je, ni lini Serikali itaajiri Wafanyakazi wa kutosha katika Idara hiyo?

(b) Je, ni lini Serikali itaimarisha Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Mjini Magharibi ili kupunguza msongamano katika Ofisi kuu ya Uhamiaji Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Machano Othman Said Mbunge wa Baraza la Wawakilishi lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Uhamiaji imetengewa Bajeti ya kuajiri Watumishi 505 katika mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika mwaka wa fedha 2017/2018 Idara ya Uhamiaji limefanya upanuzi wa Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Mjini Magharibi kwa kuongeza vyumba vitatu kwa ajili ya kuimarisha huduma za Kiuhamiaji ikiwemo huduma ya pasipoti mtandao, pia katika Bajeti ya mwaka huo Idara ya Uhamiaji imetenga fedha kwa ajili ya upanuzi wa Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Mjini Magharibi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hatua hiyo Idara itakuwa imeongeza wafanyakazi, pia Ofisi ya Uhamiaji Mjini Magharibi itaimarika ili kupunguza msongamano uliopo katika Ofisi kuu ya Uhamiaji Zanzibar.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO aliuliza:-

Je, nini Mkakati wa Serikali kuhakikisha Magereza zetu zinajitegemea kwa chakula?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Lyimo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha Jeshi la Magereza linajitosheleza kwa chakula cha wafungwa na mahabusu, Serikali imeendelea kulipatia Jeshi zana na pembejeo mbalimbali za Kilimo kupitia fedha za matumizi ya kawaida na za miradi ya maendeleo. Kwenye Bajeti ya mwaka 2018/2019 Serikali imetenga fedha kwa miradi ya maendeleo ya jumla ya shilingi Bilioni tatu kwa ajili ya ununuzi wa zana mbalimbali za Kilimo na kukamilisha miundombinu ya umwagiliaji Gereza Idete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza linaendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano wa mwaka 2018/2019 mpaka 2022/2023 kwa kutumia raslimali zilizopo ambapo katika msimu wa mwaka 2018/2019 Jeshi limelima jumla ya ekari 5,110 za mazao ya chakula kwa mchanganuo ufuatao; mahindi ekari 3,505, mpunga ekari 1,050 na maharage ekari 555 kwa matarajio ya kuvuna jumla ya tani 9,509.25.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika Awamu ya II ya utekelezaji wa Mkakati huu, Jeshi linaendelea kukamilisha andiko la Mapinduzi ya Kilimo kwa mwaka 2019/2020 na mwaka 2023/2024 likiwa na lengo la kuondokana na utegemezi wa chakula kwa wafungwa na mahabusu kutoka Serikalini.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-

Wakati Jeshi la Polisi likitekeleza majukumu yake kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na hata uvunjifu wa Katiba kwa kisingizio cha maagizo kutoka juu:-

(a) Je, ni mamlaka gani iko juu ya sheria?

(b) Je, maagizo hayo yanapopingwa na sheria za nchi na kukiuka haki za binadamu nini hukumu ya yule aliyetendewa kinyume cha sheria?

(c) Je, huyu anayekutwa na kadhia hii hana haki ya kumjua huyo mwenye mamlaka ya juu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Liwale lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi hutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo kwa msingi huo Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai Sura ya 20 inampa mamlaka polisi kutumia nguvu ya wastani anapokuwa anatekeleza kazi yake kulingana na mazingira yaliyopo. Aidha, hakuna mamlaka ya juu katika Jeshi la Polisi iliyo juu ya sheria kiasi cha kuvunja sheria.

(b) Mheshimiwa Spika, nchi yetu inafuata misingi ya Demokrasia na Utawala Bora ambapo mtu yeyote anao uwezo wa kwenda kutoa malalamiko yake kwenye chombo chochote cha kisheria na hauta stahiki zikachukuliwa.

(c) Mheshimiwa Spika, hakuna mamlaka inayomzuia mtu kumuona mtu ambaye anadhani atamsaidia kutatua tatizo Lake Linalomsibu.
MHE. SAADA MKUYA SALUM aliuliza:-

Kumekuwa na vitendo vya mauaji ya mara kwa mara kwa upande wa Zanzibar katika siku za hivi karibuni; mauaji hayo yanatokana na aidha kuuwawa kwa wanaoshukiwa kuwa ni wezi au mauaji mengine hayajulikani chanzo chake.

(a) Je, Serikali imeshafanya tathmini ya hali hiyo?

(b) Je, ni washukiwa wangapi kwa kipindi cha karibuni ambao wametiwa hatiani kutokana na vitendo vya mauaji kwa upande wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI aliji:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saada Mkuya, Mbunge wa Welezo lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwa kipindi cha hivi karibuni kumekuwa kukijitokeza mauaji ya aina mbalimbali yakiwemo yale ya wananchi kujichukulia sheria mkononi baada ya kuchukizwa na vitendo vifanywavyo na watu wanaowaua. Hali hii ni kosa kisheria na Serikali imeshafanya tathmini ya kutosha ambapo kwa kipindi cha Juni, 2016 hadi Juni, 2017 jumla ya watu 34 waliuawa, 29 kati yao waliuawa kwa kutuhumiwa wizi, mmoja kwa tuhuma za ushirikina, wawili kwa tuhuma za wivu wa mapenzi na watatu kwa migogoro ya ardhi. Thathmini hii ya Serikali inakwenda sambamba na utoaji wa elimu kwa wananchi ili wasijichukulie sheria mikononi na badala yake wawafikishe watuhumiwa mbele ya vyombo vya sheria ili kuchukuliwa hatua stahiki za kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya watuhumiwa 33 wamekamatwa kwa tuhuma za mauaji na kesi 36 zimefunguliwa na zipo katika hatua mbalimbali mahakamani na baadhi zikiwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za ujenzi wa jengo jipya la kisasa la Askari Polisi wa Makunduchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa nyumba za makazi ya askari katika eneo la Makunduchi na katika Mkoa wote wa Kusini Unguja. Eneo la Makunduchi lina jengo moja la ghorofa la makazi ya familia nne za askari lililorithiwa toka Serikali ya Mkoloni na Mahanga mawili yanayotumiwa kwa makazi ya askari. Makazi haya ni sawa na asilimia 10 tu ya mahitaji halisi. Kwa kutambua changamoto hii, Serikali imeanzisha ujenzi wa nyumba za makazi ya familia 12 za askari polisi katika Mkoa wa Kusini Unguja. Aidha, Serikali kwa kupitia jeshi la polisi na kushirikiana na wadau imeanzisha ujenzi wa kituo cha polisi cha Daraja B huko Dunga, kituo hiki kimefikia hatua za mwisho kumalizika.
MHE. HAJI KHATIB KAI aliuliza:-

Je, ni sifa gani anastahili kuwa nazo Askari Polisi ili aweze kuteuliwa kuwa OCD?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Haji Kai Mbunge wa Micheweni kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa muundo wa maendeleo ya Utumishi wa Maaifa wakaguzi na Askari wa Jeshi la Polisi ili Afisa aweze kuwa OCD ni lazima awe na sifa zifatazo;

• Awe na cheo cha Mrakibu Muandamizi wa Polisi.

• Awe na uwezo wa kuongoza ikiwa ni pamoja na kusimamia, kuratibu kazi za Maafisa, Wakaguzi na Askari walio chini yake kusimamia nidhamu katika himaya yake, kubuni na kuandaa mikakati ya ulinzi na usalama katika himaya yake.

• Awe na uwezo wa kufanya uamuzi, kutatua changamoto mbalimbali za kazi kuanzisha na kudumisha mahusiano mazuri na wananchi, pamoja na watendaji wengine wa Serikali na Taasisi zingine zilizo katika himaya yake na,

• Endapo kuna upungufu wa Maafisa wenye cheo cha Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Afisa mwenye cheo cha Mrakibu wa Polisi anaweza kupewa madaraka ya kuwa OCD ili mradi awe na uzoefu na uwezo wa kuongoza.
MHE. RUKIA KASSIM AHMED aliuliza:-

Baadhi ya magereza nchini yamejaa wafungwa na mahabusu ambao ni wakimbizi.

Je, ni lini Serikali itawarejesha wakimbizi hao makwao ili kupunguza msongamano ndani ya magereza yetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rukia Kassim Ahmed, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba miongoni mwa wafungwa na mahabusu walioko katika magereza hapa nchini ni raia wa kigeni wakiwemo wakimbizi kutoka nchi za Burudi, DRC na nchi nyingine duniani. Magereza yenye idadi kubwa ya raia wa kigeni yapo Mkoani Kigoma ambapo yana jumla ya wakimbizi 91 kati yao wafungwa 38 na mahabusu 53. Gereza la Kibondo lina wafungwa 22 na mahabusu 31, Gereza la Kasulu lina wafungwa wawili na mahabusu 19, Gereza la Bangwe lina mfungwa mmoja na mahabusu watatu, Gereza la Ilagala lina mfungwa mmoja na Gereza la Kwitengo lina jumla ya wafungwa 12. Wakimbizi ambao wamefungwa gerezani wanarejeshwa katika nchi zao za asili baada ya kumaliza kutumikia vifungo vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaendelea kuwarejesha wakimbizi nchini kwao kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wahamiaji (IOM) pamoja na nchi ya Burundi. Kuanzia mwezi wa Julai, 2018 hadi Aprili, 2019 jumla ya wakimbizi 31,643 kutoka Burundi walirejeshwa nchini kwao kwa hiyari.

Mheshimiwa Naibu Spika, idadi hiyo imefanya wakimbizi waliorejeshwa nchini mwao tangu zoezi hilo lilivyoanza mwaka 2017 hadi 2019 kufikia 66,148. Aidha, zoezi la kuwarejesha wakimbizi hao nchini kwao kwa hiari ni endelevu.
MHE. ANNA R. LUPEMBE (K.n.y. MHE. MOSHI S. KAKOSO) aliuliza:-

Wilaya ya Tanganyika haina Jengo la Polisi Makao Makuu ya Wilaya.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kituo cha Polisi eneo la Makao Makuu ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Mpanda Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Tanganyika ni miongoni mwa Wilaya mpya zilizoanzishwa na Serikali katika miaka ya hivi karibuni ambazo hazina vituo vya polisi na hata nyumba za kuishi askari.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua hitaji la Kituo cha Polisi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Tanganyika na mpango wa kujenga Vituo vya Polisi katika Makao Makuu ya Wilaya yataanza mara baada ya kufanyika kwa tathmini ya eneo husika.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-

Eneo la Rubwera Kata ya Kyerwa ndiyo Makao Makuu ya Wilaya na maeneo mengi yalikuwa ya wananchi, kuna eneo lilichukuliwa na Jeshi la Magereza na wananchi walizuiliwa kufanya shughuli yoyote kwenye eneo hilo.

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hawa kama walivyoahidiwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa wakati wa uanzishwaji wa Wilaya mpya ya Kyerwa, eneo la wananchi wa Kijiji cha Rubwera Kitongoji cha Rwekorongo lilitolewa kwa ajili ya uanzishaji wa Gereza la Wilaya. Aidha, kwa mujibu wa tathmini ya Halmashauri ya Wilaya, jumla ya shilingi 661,928,640/= zinahitajika kuwafidia wananchi waliojitolea maeneo yao mwaka 2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni nia ya Serikali kuwalipa fidia wananchi wote nchini waliotoa maeneo yao kwa ajili ya kupisha ujenzi na au uanzishaji wa magereza ikiwemo wananchi wa Rubwera. Aidha, Serikali itaendelea kulipa fidia hizo kwa wananchi kwa awamu kutegemea na upatikanaji wa fedha kutoka kwenye bajeti ya Serikali.
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA aliuliza:-

Wafanyabiashara wa Wilaya ya Kakonko wanapenda kujisajili BRELA ili kurahisisha biashara zao na kulipa kodi stahiki lakini wengi wanashindwa kufanya hivyo kwa kukosa Vitambulisho vya Taifa

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuharakisha zoezi la kutoa Vitambulisho vya Taifa ili wananchi waweze kuvitumia katika shughuli za maendeleo?

(b) Kuna wananchi wanaokaa katika mipaka kati ya Tanzania na nchi nyingine; je, Serikali imewawekea utaratibu gani wa kuwapa vitambulisho wananchi hao kwa haraka bila kuathiri malengo ya zoezi la utoaji wa Vitambulisho vya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Christopher Kajoro Chiza, Mbunge wa Buyungu, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) inaendelea kukamilisha usajili wa watu wote wenye sifa kwa matarajio ya kukamilisha zoezi la uchukuaji wa alama za vidole, picha na saini za kielektroniki ifikapo tarehe 31 Desemba, 2019. Lengo la Serikali ni kununua mashine mpya za uzalishaji wa vitambulisho zenye uwezo mkubwa zaidi ili kuharakisha upatikanaji wa Vitambulisho vya Taifa. Aidha, Mamlaka imefungua dawati Maalum la usajili katika ofisi ya BRELA, usajili huu unafanyika kwa kuzingatia sifa bila kuathiri masharti ya kisheria na kikanuni yaliyowekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuwapa vitambulisho vya taifa kwa haraka wananchi wanaokaa mikoa ya mipakani, utaratibu wake hautofautiani na utaratibu wa kawaida wa usajili ambapo mamlaka kuhakikisha kuwa taratibu zote za usajili zimezingatiwa na hatua zote za uhakiki na ufuatiliaji wa mapingamizi zimefuatwa kikamilifu. Natoa rai kwa wananchi wote nchini kuanza taratibu za usajili mapema ili kuepusha usumbufu.
MHE. BONIPHACE M. GETERE (K.n.y. MHE. VEDASTUS M. MANYINYI) aliuliza:-

Licha ya kazi nzuri ya waendesha bodaboda ya kurahisisha usafiri na kupunguza tatizo ya ajira bado ziko changamoto mbalimbali wanazosababisha kama ajali za mara kwa mara pamoja na wizi.

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza tatizo hilo?

(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kutofautisha adhabu ya waendesha bodaboda na ile ya magari makubwa kulingana na vipato vyao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, vipo vyanzo vikuu vitatu vinavyosababisha ajali za barabarani hapa nchini. Vyanzo hivyo ni makosa ya kibinadamu ambayo kuchangia kwa asilimia 76, ubovu wa magari asilimia 16 na mazingira ya barabara huchangia kwa asilimia nane. Makosa ya kibinadamu ni pamoja na uendeshaji wa kizembe/hatari, mwendo kasi, ulevi, uzembe wa wapanda pikipiki, uzembe wa wapanda baiskeli, uzembe wa watembea kwa miguu na sababu nyinginezo kama hizo.

Mheshimiwa Spika, aidha Serikali kupitia Jeshi la Polisi iimekuwa ikitoa elimu kwa waendesha bodaboda namna nzuri ya utumiaji wa pikipiki ikiwa ni pamoja na kuvaa kofia ngumu, kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa leseni za waendesha bodaboda ili kupunguza wale waendeshaji wasio na leseni ambao wanaweza kusababisha ajali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishaliona hilo na kwamba kuna hatua mbalimbali zinaendelea kufanyika ili hatimaye adhabu zitofautiane kati ya waendesha bodaboda na wale wa magari makubwa.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo kikubwa cha polisi katika Jimbo la Mtera hususani katika Kijiji cha Mvumi Misheni ili kukabiliana na wimbi kubwa la uhalifu katika Jimbo la Mtera?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi ya vijijini nchini yameongezeka idadi ya watu, shughuli zao za kiuchumi na mambo mengine ambayo yanahitaji huduma ya ulinzi na usalama toka Jeshi la Polisi ikiwa ni pamoja na Kijiji cha Mvumi Misheni.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inao mpango wa kuboresha na kujenga Vituo vya Polisi katika ngazi ya Tarafa na Kata nchi nzima ambavyo vitasaidia kusogeza huduma kwa wananchi hadi waliopo katika maeneo ya vijijini ikiwemo Kijiji cha Mvumi Misheni katika Jimbo la Mtera.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y. MHE. HAWA S. MWAIFUNGA) aliuliza:-

Ajali za barabarani bado zimekuwa tishio kubwa kwa maisha ya Watanzania, kutokana na ajali hizo tunapoteza nguvu kazi ya Taifa na familia nyingi zinabaki zikitaabika.

Je, Serikali imejipanga vipi kukabiliana na ajali hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na athari kubwa za ajali za barabarani kwa Taifa Serikali ina mkakati madhubuti wa kupambana na tatizo hili. Mikakati hiyo ni pamoja na kuongeza wigo wa elimu ya usalama barabarani kwa watumiaji wa vyombo hivyo kwa njia ya redio, luninga na machapisho na vipeperushi.

Aidha, mikakati mingine ni kuboresha mifumo ya utendaji kazi maeneo ya ukaguzi wa mabasi na maroli, mfumo wa ufuatiliaji wa magari barabarani na mfumo wa uwekaji nukta katika leseni za madereva utakaodhibiti tabia za madereva wazembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Baraza la Taifa la Usalama Barabarani Serikali ilibuni na kutekeleza mikakati hii ya kupunguza ajali barabarani ambao katika awamu tatu zilizotekelezwa mpaka sasa umefanikiwa kupunguza ajali kwa asilimia 43. Aidha, awamu ya nne ambayo inaendelea kutekelezwa tumejipanga kupunguza ajali kwa asilimia 35.
MHE. SHALLY J. RAYMOND (K.n.y. MHE. ZAINAB A. KATIMBA) aliuliza:-

(a) Je, Serikali ipo tayari kuwaeleza Watanzania hususani vijana kuwa hatua gani zimechukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuwabaini, kuwachunguza na hatimaye kuwahukumu wale wote waliobainika kujihusisha na mtandao wa biashara za dawa za kulevya?

(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia vijana waliotumbukia kwenye dimbwi la matumizi ya dawa za kulevya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Naibu Spika, tokea Awamu ya Tano iingie madarakani imewabaini na kuwakamata watuhumiwa kama ambavyo inaorodheshwa hapa chini. Watumiaji wa dawa za kulevya za viwandani mwaka 2016 idadi ya makosa ni 679 na watuhumiwa waliokamatwa ni 1,269 ambao kati ya hao wanaume ni 1,127 na wanawake 142; mwaka 2017 idadi ya makosa ni 902 ambapo watuhumiwa 1,578 walikamatwa kati ya hao 1,485 ni wanaume na 93 ni wanawake; mwaka 2018 makosa yalikuwa ni 702 ambapo watuhumiwa 886 walikamatwa kati ya hao 796 ni wanaume na wanawake walikuwa 90 na mwezi Januari, 2019 hadi Machi, 2019 jumla ya makosa yalikuwa ni 133, watuhumiwa waliokamatwa ni 174 kati ya hao 162 ni wanaume na 12 ni wanawake.

Mheshimiwa Naibu Spika, madawa ya mashambani kwa maana ya mirungi na bangi; mwaka 2016 jumla ya makosa ya madawa ya mashambani ni 10,375 ambapo watuhumiwa walikuwa ni 26,031, kati ya hao wanaume 23,872 na watuhumiwa wanawake walikuwa 2,159; mwaka 2017 makosa ya madawa ya kulevya yalikuwa ni 8,956 na watuhumiwa walikuwa 12,529 wakati wanaume walikuwa 12,529 na wanawake walikuwa ni 1,112; mwaka 2018 makosa yalikuwa ni 7,539 watuhumiwa walikuwa 9,987 ambapo wanaume walikuwa ni 8,935 na wanawake walikuwa ni 1,052 na Januari, 2019 hadi Machi, 2019 makosa yalikuwa 1,842 ambapo wanaume walikuwa 2,340 na wanawake walikuwa 202.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi watuhumiwa wamepelekwa mahakamani na wengine upelelezi wa kesi zao na mashauri yao unaendelea na uko kwenye hatua tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi kupitia programu ya kuzuia uhalifu limeendelea kutoa huduma ya urekebishaji kwa waathirika wa dawa za kulevya kwa kutumia vikundi mbalimbali kama vile vya michezo nchini chini ya miradi ya kuzuia uhalifu kama vile familia yangu haina uhalifu na klabu ya usalama kwetu wetu kwanza.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI (K.n.y MHE. STANSLAUS S. MABULA) aliuliza:-

Magari mengi ya Serikali yanafanyiwa service kwenye gereji kubwa hapa nchini hii imekuwa tofauti kwa magari yanayomilikiwa na Jeshi la Polisi:-

Je, Serikali haioni kuwa upo umuhimu wa kuwa na maeneo ya kutengeneza na kurekebisha magari ya Polisi ili kuliimarishia vitendea kazi.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linayo karakana kuu ya kutengeneza na kurekebisha magari yake iliyopo barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam. Karakana hii ina matawi katika kila Mkoa nchini nzima, matawi hayo kufanya kazi kwa utaratibu wa Jeshi la Polisi chini ya Komandi ya karakana kuu iliyopo Dar es Salaam ambako kuna mafundi wenye ujuzi mkubwa. Aidha, Jeshi la Polisi kupitia makubaliano ya kimkataba kuna baadhi ya magari ya Jeshi la Polisi hutengenezwa katika karakana za wazabuni waliokubaliana baada ya kupata kibali cha TEMESA.
MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto za kiusalama katika Jimbo la Singida Kaskazini kutokana na jiografia yake na rasilimali zilizopo:-

Je, ni lini Serikali itaongeza Vituo vya Polisi katika Kata ya Mughunga, Mgori na Merya ili kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uhaba wa vituo vya Polisi nchini ikiwemo Kata za Mughunga, Mgori na Merya. Hata hivyo huduma za kiusalama kwa wananchi wa Kata hizo zinatolewa na vituo vya Polisi vya Misange na Ngimwa kwa uratibu wa kituo cha Polisi cha Wilaya ya Singida Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ujenzi wa vituo vya Polisi kwa nchi nchi nzima unahitaji rasilimali fedha nyingi, Jeshi la Polisi limeweka vipaumbele vya kiusalama katika kutekeleza ujenzi wa vituo hivyo ikiwemo katika Kata ya Mughunga, Mgori na Merya na kadhalika kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo wananchi.
MHE. DKT. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-

Mwaka 2017/2018 kulitokea mauaji ya vijana wa bodaboda katika Wilaya ya Masasi ambapo vijana wanaokaribia kuwa zaidi ya kumi wameuwawa kikatili na kunyang’anywa pikipiki:-

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu matukio haya katika Wilaya ya Masasi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kweli kuwa kulikuwa na mauaji ya vijana zaidi ya 10 katika Wilaya Masasi. Kwa mwaka 2017/2018 kulikuwa na matukio manne ya mauaji yaliyotokea na kuripotiwa katika vituo vya Polisi Wilaya ya Masasi. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kutokomeza uhalifu huo kwa kuwakamata watuhumiwa wote ambao wamekuwa wakijihusisha na uhalifu wa aina mbalimbali ikiwemo mauaji. Hatua hizi ni pamoja na kufanya doria na misako ya mara kwa mara katika maeneo tofauti katika Wilaya ya Masasi kutoa elimu kwa waendesha bodaboda juu ya tahadhari ya kuwabeba abiria usiku na kushirikisha jamii yote katika kuwafichua wahalifu walio kati yao ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-

Kituo cha Polisi Nkome kina Askari wa kiume pekee hivyo hata huduma kwa akina Mama ikiwemo upekuzi hufanywa na Askari wa kiume:-

Je, ni lini sasa Serikali itapeleka askari wa kike katika kituo hicho?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vituo vidogo vya Polisi Nkome, Nyamboge, Kakubilo na Nzela ni vituo vilivyo katika maeneo ambayo yanakaribiana na kutokana na changamoto za mazingira magumu na ukosefu wa mazingira rafiki, vituo hivi kwa sasa havina Askari wa Kike ambao wanaishi na kufanya kazi. Hata hivyo, vituo hivi kupata doria maalum kila mara kutoka Kituo Kikuu cha Polisi Wilaya ya Geita ambapo Askari wa Kike na Kiume hufika na kutoa huduma za kiusalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, endapo kuna mtuhumiwa wa kike amekamatwa katika vituo hivi vidogo hufanyika utaratibu wa kumpata mgambo wa kike wa eneo hilo au mwanamke yeyote mtu mzima mwenye busara anayepatikana kwa urahisi katika maeneo hayo kama ambavyo PGO 288 (8), (a) inavyoelekeza, ambapo hufanya upekuzi kwa mtuhumiwa huyo mwanamke.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kweli kuwa watuhumiwa wa kike hupekuliwa na Askari wa Kiume, Serikali itapeleka Askari wa Kike pindi mazingira ya utendeji kazi hususan makazi yatakapokuwa yameboreshwa.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Kituo cha Polisi Lukumbule kiliungua moto miaka iliyopita na mpaka sasa kituo hicho hakina Askari kimefungwa:-

(a) Je, ni lini Serikali itakirejesha kituo hicho hasa ikizingatiwa kuwa kipo mpakani mwa nchi ya Msumbiji?

(b) Je, ni lini Serikali itaweka kituo cha Uhamiaji katika kituo hicho cha Lukumbule?

(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia ujenzi wa Kituo cha Polisi Lukumbule ambacho kimeishia kwenye lenta baada ya Halmashauri kushindwa kumalizia ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Idd Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Lukumbule kilichomwa moto mwaka 2013 na baadhi ya wananchi wasiotaka kutii sheria katika eneo hilo. Baada ya tukio hilo Jeshi la Polisi kwa kutambua kwamba eneo husika ni la mpakani na nchi ya Msumbiji limekuwa likifanya doria za mara kwa mara na pia kushirikisha taasisi nyingine za Serikali ambazo ni wadau wa ulinzi na usalama katika kuimarisha hali ya ulinzi na usalama kwa wananchi wa eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa kufungua Kituo cha Uhamiaji Kata ya Lukumbule upo kwenye hatua za mwisho na inatarajiwa kufanguliwa wakati wowote mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuupongeza uongozi wa Halmashauri ya Tunduru kwa ujenzi wa kituo cha Polisi cha Lukumbule ingawa bado ujenzi wake haujakamilika. Hata hivyo, Serikali inatambua umuhimu na uhitaji wa kituo cha Polisi katika eneo hilo. Aidha Serikali kupitia Jeshi la Polisi itafanya tathmini ili kubaini gharama halisi za kukamilisha sehemu ya ujenzi uliobakia na kuona uwezekano wa kukamilisha ujenzi huo.
MHE. USSI SALUM PONDEZA AMJADI aliuliza:-

Vituo vingi vidogo vya Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja vimefungwa na kuwapa wakati mgumu wananchi wanapohitaji huduma ya polisi wakati vilikuwa vinasaidia kupambana na uhalifu kwa wakati muafaka:-

(a) Je, ni kwa sababu gani vituo hivyo vimefungwa na wananchi kulazimika kupata huduma katika vituo vikubwa kinyume na malengo ya kuanzishwa kwake?

(b) Je, ni kwa nini vituo vya Kilimani, Mkunazini, Mlandege pamoja na vituo vingine vimefungwa na wananchi kulazimika kufuata huduma umbali mrefu?

(c) Je, hatua ya kufunga vituo hivyo inasaidia vipi katika kupambana na uhalilfu hasa katika maeneo ya katikati ya mji wa Zanzibar na Serikali ina mpango gani na majengo yake?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Vituo vya Polisi vimegawanyika katika madaraja matatu, ambayo ni Daraja A, B na C. Utendaji kazi wa vituo hivi unazingatia Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi (POG). Mathalani, kwa mujibu wa PGO 287(2), vituo Daraja A na B vinatakiwa kufunguliwa na kufanya kazi saa 24 na vituo Daraja C vinatakiwa kufunguliwa na kufanya kazi saa 12 tu kuanzia saa 12.00 asubuhi hadi 12.00 jioni.

(b) Mheshimiwa Spika, vituo ambavyo havitumiki kwa sasa ikiwemo vituo vidogo vya Mwembeladu, Shaurimoyo na Forodhani inatokana na sababu mbalimbali ikiwemo uchakavu, vipaumbele kwenye mgawanyo wa rasilimali watu na kadhalika. Aidha, kwa sasa maeneo hayo ambayo yalikuwa yanahudumiwa na vituo hivyo yanahudumiwa na vituo vikuu ya polisi vilivyo karibu.

(c) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inapambana na vitendo vya uhalifu maeneo ya katikati ya Mji wa Zanzibar kwa kuimarisha ulinzi, misako na doria.
MHE. HASNA S. K. MWILIMA aliuliza:-

Vijana wengi wa maeneo ya Nguruka na Uvinza kwa ujumla biashara zao ni pikipiki na Polisi wamekuwa wakiwakamata na kuwatoza faini nyingi vijana hao bila utaratibu:-

Je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati wa kulielekeza Jeshi la Polisi kuacha mara moja kuwasumbua vijana hao wa bodaboda ambao wanajipatia kipato kupitia bodaboda?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, pikipiki za matairi mawili (bodaboda) na matatu (bajaji) zilianza kutumika kubeba abiria kuanzia mwaka 2008 Tanzania Bara na mwaka 2009 Bunge la Jamhuri ya Muugano wa Tanzania iliridhia vyombo hivyo vitumike kutoa huduma ya usafirishaji wa abiria.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua biashara inayofanywa na pikipiki za kubeba abiria na inathamini mchango wao katika kutoa huduma hiyo ambayo imesaidia sana katika kutoa ajira katika mikoa yote Tanzania Bara. Hata hivyo, si wote ambao wanakiuka Sheria za Usalama Barabarani na Kanuni zake.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi limekuwa likichukua hatua dhidi ya waendesha bodaboda wote ambao wamekuwa hawazingatii sheria, kanuni na masharti ya leseni za usafirishaji ikiwa ni pamoja na wapanda pikipiki wa maeneo ya Nguruka na Uvinza. Aidha, Serikali imekuwa ikiendelea kutoa mafunzo kwa waendesha bodaboda juu ya matumizi bora ya barabara.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-

Azma ya Serikali ya kuwafikishia wananchi huduma popote walipo ni njema. Aidha, naipongeza Serikali kwa ujenzi wa Kituo kipya cha Polisi Dunga baada ya jengo la awali kuwa bovu na kuvunjwa.

(a) Je, ni lini jengo hilo jipya litakamilishwa kwa kufanyiwa matengenezo yaliyobaki?

(b) Je, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi iko tayari kukipatia Kituo cha Polisi Dunga gari la huduma?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Kituo cha Polisi Dunga Daraja C ulianza mwezi Julai, 2018 na ulisimama mwezi Novemba, 2018 ukiwa umefikia hatua ya umaliziaji (finishing) ambayo tathmini yake inakadiriwa kufikia shilingi 49,862,220.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi linategemea kupata fedha hizo kutoka katika Mfuko wa tuzo na tozo na zitatumiwa katika mfumo wa nguvu kazi (Force Account).

(b) Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi Dunga kipo katika Wilaya ya kati Mkoa wa Kusini Unguja. Mkoa mzima una jumla ya magari ya Polisi 17. Wilaya ya kati peke yake ina magari mawili mazima. Jeshi la Polisi limekuwa likigawa magari kwa awamu kwa kadiri yanavyopatikana. Kituo cha Polisi Dunga ni miongoni mwa vituo vitakavyopatiwa magari pindi yatakapopatikana.
MHE. ISSA J. MTEMVU Aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza kikamilifu Waraka Na. 3 wa mwaka 2015 kuhusu Muundo wa Kada ya Uhasibu na Ukaguzi wa Ndani?

(b) Je, ni lini Kitengo cha Uhasibu na Fedha katika Wizara na Sekretarieti za Mikoa zitapewa hadhi ya kuwa Idara?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima pamoja na afya njema. Pia nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa imani yake aliyokuwa nayo kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, nijibu swali la Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Waraka Na. 3 wa mwaka 2015 kuhusu Muundo wa Kada ya Uhasibu na Ukaguzi wa Ndani ulianza kutekelezwa mwezi Julai, 2018 kwa kutenganisha Kada ya Maafisa Hesabu na Wahasibu. Kwa mujibu wa muundo huo mpya Wahasibu na Wakaguzi ni wale ambao wana CPA na wale wasio na CPA wanatambulika kama Maafisa Hesabu na Maafisa Ukaguzi.

(b) Mheshimiwa Spika, kuhusu kupandisha hadhi vitengo vya uhasibu na fedha katika Wizara na Sekretarieti za Mikoa kuwa idara, katika kuandaa miundo ya taasisi, vigezo kadhaa hutumika ili kufikia maamuzi ya kuwa Idara, Vitengo na Sehemu. Kwa kuwa miundo hii hufanyiwa marekebisho mara kwa mara kwa kushirikiana na wataalamu wa miundo kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na kujadiliwa katika ngazi ya maamuzi, ni mategemeo yetu kwamba Serikali itakapoona kuwa Kitengo cha Uhasibu na Fedha kinakidhi vigezo vya kuwa idara, kitapewa hadhi hiyo.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza:-

Je, wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja uliofanywa na mtumishi wa benki ni nani mwenye wajibu wa kumlipa mteja?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan Omar King, Mbunge wa Jang’ombe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja, uchunguzi wa kina hufanywa na vyombo husika katika masuala ya upelelezi ikiwa ni pamoja na Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa kadri hali na mazingira ya tukio yatakavyokuwa yametokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, endapo ikibainika kuwa wizi huo umefanywa na mtumishi wa benki, hatua stahiki huchukuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo ikiwa ni pamoja na mteja kulipwa kiasi cha fedha alichoibiwa na mhalifu kuchukuliwa hatua za kinidhamu pamoja na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria. Pia, Benki Kuu hutoa adhabu kwa benki husika pale inapobainika kwamba utaratibu uliowekwa na benki husika ulikuwa na kasoro zilizochangia kuibiwa kwa fedha za mteja.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kufuta madeni ya muda mrefu kwa wafanyabiashara wa ndani yatokanayo na ukosefu wa elimu juu ya matumizi sahihi ya mashine za EFD wanayodaiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali ilitoa msamaha kwa wadaiwa wa kodi ili kuongeza makusanyo. Msamaha huu ulihusisha riba na adhabu zilizoambatana na madeni yote yaliyolimbikizwa kwa miaka ya nyuma. Msamaha huu ulilenga kusamehe malimbikizo ya nyuma ya riba na adhabu kwa kiwango cha asilimia 100 kwa wafanyabiasha wote hapa nchini ambao walikuwa na malimbikizo ya madeni ya kodi. Msamaha huo ulitolewa kwa kipindi cha miezi sita kilichoanzia tarehe 1 Julai, 2018 mpaka tarehe 31 Desemba, 2018 ambapo kutokana na kusuasua kwa utekelezaji wake, Serikali iliongeza muda wa msamaha huo kwa miezi sita ili wafanyabiashara waliokuwa na madeni hayo kuweza kukamilisha malipo husika yaliyotokana na msamaha huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hiyo ya marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Kodi Sura 438 ilitarajiwa kuongeza mapato ya Serikali na kukusanya malimbikizo ya madeni ya nyuma ya kodi pamoja na kuinua kiwango cha ulipaji kodi kwa hiyari kwa zaidi ya asilimia 10.

Hata hivyo, licha ya nia nzuri ya Serikali ya kufuta riba na adhabu ili kuwawezesha walipa kodi wenye madeni sugu ya kodi kuyalipa kwa awamu ili kurahisisha mwendelezo wa biashara zao, wengi wao hawakulipa kodi hizo hata baada ya kuingia mikataba na TRA na hata baada ya Serikali kuongeza muda wa ziada wa kufanya malipo ya kodi husika yaliyotokana na msamaha huo. (Makofi)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua Ofisi Ndogo ya Hazina Zanzibar kama ilivyo kwa taasisi nyingine za Muungano ili kurahisisha huduma kwa wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wanaoishi Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan Omar King, Mbunge wa Jang’ombe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huduma za malipo ya mafao ya wastaafu wanaolipwa na Wizara ya Fedha na Mipango hufanyika kupitia Ofisi za Hazina Makao Makuu, Dodoma. Aidha, Ofisi za Hazina Ndogo zilizopo katika Mikoa ya Tanzania Bara hutumika kwa ajili ya kukusanya hoja za wastaafu na kuziwasilisha Hazina Makao Makuu, Dodoma.

Mheshimiwa Spika, kwa wastaafu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanaoishi Zanzibar, Wizara ya Fedha na Mipango ya Serikali ya Muungano wa Tanzania mara zote imekuwa ikifanya kazi kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa ajili ya kupokea hoja za madai ya wastaafu hao na kuziwasilisha Hazina Makao Makuu, Dodoma kwa ajili ya taratibu za malipo.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha na Mipango ya Serikali ya Muungano wa Tanzania itaimarisha ushirikiano na Wizara ya Fedha na Mipango ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuwahudumia wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wanaoishi Zanzibar kama ambavyo hushirikiana na Ofisi za Hazina Ndogo zilizopo Tanzania Bara.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE K.n.y. MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kutatua changamoto ya msongamano wa magari yanayovuka kuelekea nchi jirani kupitia mpaka wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari katika Kituo cha Forodha Tunduma. Hatua hizo ni pamoja na kutekeleza mpango wa kurasimisha utaratibu wa kubadilishana taarifa za mizigo kati ya Dar es Salaam na Nakonde, Zambia; kuendelea kutoa huduma za forodha kwa muda wa saa 24; kuimarisha mifumo ya TEHAMA ya pande mbili ili kuwezesha taarifa za mizigo inayotoka katika Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia kusomana kwa wakati; na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa makubaliano baina ya pande mbili ya Januari, 2020 kuhusu mkakati wa kuboresha miundombinu ya barabara pamoja na ujenzi wa maeneo ya maegesho ya magari kwa upande wa Zambia.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Zambia zitaendelea kuimarisha utendaji wa taasisi zote zinazohusika na shughuli za forodha katika Kituo cha Tunduma, pamoja na kuboresha mifumo ya TEHAMA na miundombinu ya barabara ili kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza: -

(a) Je, ni wakulima wangapi wadogo wadogo wamepata mikopo kutoka Benki ya Kilimo ili kukuza tija kwa wakulima hao?

(b) Je, riba za Benki ya Kilimo zinatofauti gani na riba za Benki za Biashara katika kumsaidia mkulima mdogo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Julai, 2021 Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) imekwishatoa mikopo yenye jumla ya shilingi bilioni 281.74 kwa ajili ya kuendeleza miradi ya kilimo, ufugaji na uvuvi nchini. Mikopo hiyo imewanufaisha wakulima 1,514,695 vikiwemo vyama vya wakulima 151 hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, sambamba na utoaji wa mikopo ya moja kwa moja, Benki ya Maendeleo ya Kilimo inasimamia Mfumo wa Dhamana kwa Wakulima Wadogo (Smallholder Credit Guarantee Scheme – SCGS) unaolenga kuchagiza mabenki na taasisi za fedha kuongeza ukopeshaji katika sekta ya kilimo. Hadi kufikia mwisho wa mwezi Juni 2021, SCGS ilitoa udhamini wa mikopo kwa wakulima wadogo 11,244, vikundi vya wakulima 181 na SMEs 43 waliopata mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 89.92 kutoka benki 9 washiriki katika uendeshaji wa mfuko wa SCGS.

(b) Mheshimiwa Spika, kwa upande wa riba, Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) imeweka utaratibu wa kutoza riba kwa kiwango cha asilimia 10 kwa kuzingatia uwezo wa wazalishaji wa madaraja tofauti katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi. Kwa maana hiyo, mikopo inayotolewa kwa wakulima wadogo hutozwa riba nafuu isiyozidi asilimia 10 na kwa masharti nafuu ya urejeshwaji wake yanayozingatia misimu ya mavuno na mauzo ya mazao.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhuisha vigezo vya mfumo wa miradi ya kimkakati kupitia maandiko ya miradi ili iweze kusaidia Halmashauri kubuni miradi ya kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejikita katika kutoa huduma bora na zenye uhakika kwa wananchi wake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba Mamlaka za Serikali za Mitaa zinaendelea kujiongezea mapato kwa kutumia fursa zilizopo katika maeneo yao ili kutoa huduma bora kwa lengo la kupunguza utegemezi wa ruzuku kutoka Serikali Kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufikia lengo hili, Serikali iliandaa mkakati maalum wa kuwezesha halmashauri kujitegemea kimapato. Katika kutekeleza mkakati huo, Mamlaka za Serikali za Mitaa zinatakiwa kuhakikisha zinatumia kwa ukamilifu fursa za kimapato zilizopo katika maeneo yao na kuongeza uwezo wa kujitegemea kimapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za kugharamia miradi ya kimkakati hutolewa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na Wizara ya Fedha Mipango. Hivyo, hoja ya Mheshimiwa Mbunge kuhusu uboreshaji wa vigezo vilivyowekwa kwenye uchambuzi wa miradi ya kimkakati imechukuliwa na kwa sasa Serikali inaangalia njia bora itakayosaidia kuboresha utaratibu wa maombi na vigezo vya uandaaji wa miradi ya kimkakati kabla ya utoaji wa fedha.
MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza: -

Je, ni nini hatma ya biashara ya maduka ya kubadilisha fedha (Bureau de Change) yaliyofungwa na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ukaguzi ambao umefanyika mwaka 2018/2019 ulisababisha maduka mengi ya kubadilisha fedha za kigeni kufungwa kutokana na kubainika kuendesha biashara bila kuzingatia sheria na kanuni husika. Baada ya kufungwa kwa maduka hayo, benki za biashara nchini zilihamasishwa kuendelea kutoa huduma ya kubadilisha fedha za kigeni katika matawi yake yote nchini. Kwa sasa benki zote za biashara zinatoa huduma hizo nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, pia maduka ambayo hayakufungwa yameendelea kufungua matawi na kutoa huduma hizo katika miji mbalimbali nchini. Kwa ujumla hali ya upatikanaji wa huduma ya kubadilisha fedha za kigeni nchini ni ya kuridhisha. Aidha, maduka yaliyofungwa pamoja na kampuni nyingi ambayo yanayotaka kufanya biashara ya kubadilisha fedha za kigeni nchini, yanaruhusiwa kuomba leseni Benki Kuu kwa kuzingatia matakwa ya Sheria za Fedha za Kigeni ya mwaka 1992 pamoja na Kanuni za Biashara ya Kubadilisha Fedha za Kigeni ya mwaka 2019. Hadi kufikia tarehe 30 Julai 2021, Benki Kuu ilikuwa imepokea maombi mapya manne ya leseni ya biashara ya kubadilisha fedha za kigeni ambazo yanafanyiwa uchambuzi na wahusika watapewa leseni iwapo watakuwa wamekidhi vigezo.
MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza Kodi kwenye Vifaa vya Mchezo ili Sekta ya Michezo iweze kustawi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakaposa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 Serikali kwa kuona umuhimu wa Sekta ya Michezo nchini, imetoa msahama wa Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye nyasi bandia kwa viwanja vya mpira vilivyopo kwenye Manispaa na Majiji.

Aidha, Serikali itaendelea kutoa msamaha wa VAT kwenye nyasi bandia kwa viwanja vya mpira vilivyopo kwenye Halmashauri baada ya kuridhishwa na matumizi ya msamaha uliotolewa kwenye Manispaa na Majiji. Aidha, katika kuendeleza Sekta ya michezo nchini Serikali imetoa msamaha wa VAT kwenye huduma za elimu zitolewazo kwenye vituo vya mafunzo ya michezo nchini.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha mpaka wa Kirongwe kwa kujenga One Border Post ili kuimarisha na kuongeza mapato ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kuboresha mpaka wa Kirongwe kwa kuweka miundombinu wezeshi itakayotoa kutoa huduma kwa pamoja. Aidha, katika mwaka 2021/2022, Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi million 407 kwa ajili ya usanifu na ujenzi wa nyumba za makazi za watumishi Kirongwe. Vilevile, katika mwaka 2022/2023 Serikali imepanga kuboresha mipaka mbalimbali nchini ikiwemo mpaka wa Kirongwe ili taasisi za Serikali ziweze kutoa huduma kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuimarisha mipaka yetu kwa kujenga nyumba za makazi kwa watumishi wa taasisi zinazofanya kazi mipakani na ofisi za kutolea huduma kwa pamoja mipakani ili kuboresha ulinzi na usalama wa nchi na pia kuongeza mapato ya Serikali.
MHE. VITA R. KAWAWA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwarudishia wamiliki halali silaha zao ambazo zilichukuliwa na Serikali wakati wa zoezi la Operesheni Tokomeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, Mbunge wa Jimbo la Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo mwaka 2013, Serikali baada ya kuona matukio ya ujangili na uwindaji haramu umeongezeka hapa nchini, hasa kwenye hifadhi za Taifa na mapori tengefu, iliendesha Operesheni Tokomeza na lengo lake lilikuwa kuwasaka na kuwakamata majangili pamoja na silaha walizokuwa wakizitumia. Operesheni hiyo ilishirikisha TAWA pamoja na vikosi vya ulinzi na usalama na jumla ya silaha 1,579 zilikamatwa na mpaka sasa zinashikiliwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 7 Januari, 2017 Serikali kupitia Wizara za Kisekta ambazo ni Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Wizara ya Katiba na Sheria, walikubaliana kwa pamoja silaha hizo zisirudishwe kwa wamiliki mpaka itakapofanyika tathmini ya hitaji la kuwarejeshea wamiliki wa silaha hizo. Nakushukuru.
MHE. OMAR ALI OMAR aliuliza: -

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati jengo kongwe la Polisi Wete ambalo lipo katika hali mbaya?

(b) Je, ni lini Serikali itayatengeneza magari ya polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo kwa sasa ni gari moja tu linafanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omar Ali Omar, Mbunge wa Jimbo la Wete swali lake lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uchakavu wa jengo la Kituo cha Polisi Wete ambalo limejengwa mwaka
1973. Tathmini kwa ajili ya ukarabati ilifanyika mwaka 2021 na kubaini kwamba kiasi cha shilingi 52,760,000 kinahitajika ili kugharamia ubadilishaji paa, mfumo wa umeme, ceiling board pamoja na kupaka rangi. Hivi sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Kaskazini Pemba kuna magari ya polisi 12 na yanayofanya kazi ni magari matano na magari saba ni mabovu. Tayari magari hayo yameshafanyiwa tathmini ya ubovu na kubainika kuwa kiasi cha shilingi 44,254,000 kinahitajika kwa ajili ya ukarabati. Aidha, ukarabati huo utafanyika kulingana na upatikanaji wa fedha. Nakushukuru.
MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia ujenzi wa Kituo cha Polisi Galapo Tarafa ya Babati ambacho kinajengwa kwa nguvu za Wananchi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mara baada ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani yake na nimwahidi kuwa sitamwangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mhesimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua na kuthamini michango na jitihada zinazofanywa na wananchi, Wabunge na Viongozi wengine katika kuchangia masuala ya ulinzi na usalama katika maeneo yao. Kituo cha Polisi cha Galapo kimejengwa kwa nguvu za wananchi na kwa sasa kimeshapauliwa na kazi iliyobaki ni kuweka milango, madirisha, kupiga plasta, kuweka sakafu pamoja na kupaka rangi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inawapongeza sana wananchi wa Galapo pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwa jitihada zao zilizowezesha ujenzi huo. Kwa njia ya kuunga mkono jitihada hizo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi itatumia fedha kutoka kwenye Mfuko wa Tuzo na Tozo katika mwaka wa fedha 2022/2023 ili kukamilisha ujenzi huo.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza: -

Je ni lini Serikali italeta Bungeni Muswada wa Sheria ya Kampuni Binafsi za Ulinzi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Athuman Almasi Maige, Mbunge Wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwepo kwa Sheria inayosimamia Makampuni Binafsi ya Ulinzi na kwa sasa Waraka wa Baraza la Mawaziri kuhusu mapendekezo ya kutunga Sheria ya Huduma za Sekta Binafsi ya Ulinzi umekamilika na utawasilishwa katika Baraza la Mawaziri kwa ajili ya maamuzi baada ya kupata maoni ya kina ya wadau wa pande zote mbili za Muungano juu ya rasimu ya sheria hiyo. Baada ya kukamilika kwa hatua hizo Muswada wa Sheria hiyo utaletwa Bungeni.
MHE. BAHATI K. NDINGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka mfumo utakaoruhusu wafungwa kupata haki ya faragha na wenza wao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutoa haki mbalimbali kwa wafungwa walioko magerezani kwa mujibu wa sheria. Haki ya faragha kwa wafungwa na wenza wao itaanza kutolewa pale ambapo mifumo ya kisheria, na miundo mbinu ya magereza itakapokidhi kutolewa kwa haki hiyo. Masuala mengine yatakayozingatiwa ni usalama, mila na desturi za Watanzania, kwani haki hiyo inatakiwa kutekelezwa kwa faragha.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti ongezeko la uhalifu nchini?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inaendelea na mikakati yake ya kudhibiti vitendo vya uhalifu hapa nchini kwa kuimarisha doria, kufanya misako na operesheni mbalimbali dhidi ya uhalifu na wahalifu, pamoja kutoa elimu kwa jamii kutokujihusisha na vitendo vya uhalifu na kufuata sheria za nchi. Kushirikisha jamii kwenye ulinzi wa maeneo yao kupitia dhana ya ulinzi shirikishi. Pia Serikali imewapeleka wakaguzi wa polisi kwenye kata na shehia ili kushughulikia uhalifu kwa kushirikiana na wananchi.
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawapatia Vitambulisho vya Taifa na vyeti vya kuzaliwa wananchi wa Kata za Ololosokwan, Soitsambu na Enguserosambu Ngorongoro?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Shangai Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Agosti 2022 jumla ya wananchi 84,637 katika Wilaya ya Ngorongoro wametambuliwa na kusajiliwa. Namba za Utambulisho 61,237 ambayo ni sawa na asilimia 72.3 ya wananchi wote waliotambuliwa na kusajiliwa zimezalishwa na kugawiwa kwa wananchi. Aidha, jumla ya vitambulisho 46,997 ambayo ni sawa na asilimia 76.7 ya namba za utambulisho tajwa vimezalishwa pamoja na kugawiwa kwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, usajili na utambuzi wa wananchi na uzalishaji na ugawaji Vitambulisho vya Taifa ni kazi endelevu. Hivyo, Mamlaka itaendelea na usajili wa wananchi wanaokidhi vigezo kupitia ofisi za usajili wa wilaya pamoja na kuzalisha na kugawa Vitambulisho vya Taifa kwa wananchi kupitia katika kata zote.

Mheshimiwa Spika, usajili na utoaji wa vyeti vya kuzaliwa bila malipo unaendelea katika vituo vyote vinavyotoa huduma ya afya ya mama na mtoto pamoja na vituo vya kata.
MHE. MOHAMED ABDULRAHMAN MWINYI aliuliza: -

Je, ni lini Wananchi wa Wilaya ya Mkoani waliosajiliwa kwa muda mrefu watapewa Vitambulisho vya NIDA?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohammed Abdulrahman Mwinyi, Mbunge wa Jimbo la Chambani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa imeandikisha jumla ya wananchi 47,557 ambayo ni sawa na asilimia 94 ya waliokadiriwa kuandikishwa katika Wilaya ya Mkoani. Aidha, Namba za Utambulisho 45,785 zilizalishwa sawa na asilimia 96 ya wananchi wote walioandikishwa.

Mheshimiwa Spika, jumla ya vitambulisho 41,494 ambayo ni sawa na asilimia 91 ya Namba za Utambulisho vimegawiwa kwa wananchi wa Wilaya ya Mkoani. Aidha, mwezi Septemba, 2022 jumla ya vitambulisho 1,000 vimepelekwa Wilaya ya Mkoani ili vigawiwe kwa wananchi. Serikali itaendelea kuzalisha vitambulisho na kuvigawa kwa wananchi walioandikishwa.
MHE. MAULID SALEH ALI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzuia Hati za kusafiria kwa Wakandarasi wanaoingia nchini kutekeleza miradi mbalimbali?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Saleh Ali, Mbunge wa Welezo, kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Spika, Serikali haina mkakati wa kuzuia hati za kusafiria kwa Wakandarasi wanaoingia nchini kutekeleza miradi mbalimbali isipokuwa inafanya hivyo kwa mujibu wa sheria pale inapohitajika. Serikali kupitia Sheria ya Uhamiaji Sura Na. 54 rejeo la mwaka 2016, imeipa mamlaka Idara ya Uhamiaji kuweza kushikilia au kuzuia kitu chochote ikiwa ni pamoja na nyaraka yoyote ambayo inaweza kuonyesha au kuthibitisha uvunjifu wa sheria.
MHE. CECILIA D. PARESSO aliuliza: -

Je, nini kauli ya Serikali katika kutatua changamoto ya wimbi kubwa la mauaji hapa nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge Wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Spika, ni kweli kumekuwa na ongezeko la matukio ya mauaji hapa nchini. Matukio mengi yanasababishwa na wananchi kwanza kujichukulia sheria mikononi mwao, lakini pili ni wivu wa mapenzi, lakini zaidi migogoro ya ardhi, ulevi na imani za kishirikina.

Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti wimbi hili tuliunda tume maalum ya kuchunguza na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukua, pamoja na kuchukua hatua za kisheria kama zilivyopendekewa na tume tuliyoiunda, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kwa kuwashirikisha viongozi wa siasa, dini, wazee wa mila na watu wanaoheshimika kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za nchi, katika kutatua migogoro na migongano katika jamii. Nashukuru.
MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je, ni kesi ngapi za wakulima kulishiwa mazao yao zimeripotiwa na ngapi zimepelekwa mahakamani katika Wilaya ya Kilosa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kesi zilizoripotiwa polisi za wakulima kulishiwa mazao yao Wilayani Kilosa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2018 hadi 2022 ni kesi 1,403. Katika kesi hizo zilizofikishwa mahakamani ni 1,037 na zilizotolewa hukumu na mahakama ni kesi 540.

Mheshimiwa Spika, vilevile kesi 356 ziliondolewa ama kufutwa mahakamani kutokana na sababu mbalimbali. Nakushukuru.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kununua magari ya Polisi kwa ajili ya vituo vya Polisi nchini?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu na uhitaji wa kulipatia Jeshi la Polisi magari kama nyenzo za kutendea kazi. Kupitia mkataba kati ya Serikali na Kampuni ya Ashok Leyland ya nchini India, Serikali inategemea kupokea magari 369 kutoka nchini India ifikapo Septemba, 2022 ambapo mwishoni mwa mwezi Aprili, 2022 tunatarajia kupokea magari 78 yameshakaguliwa na kuthibitishwa. Magari hayo yatakapofika yatagawiwa kwenye Vituo vya Polisi vyenye uhitaji mkubwa.
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: -


Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kujenga vituo vya Polisi katika maeneo mbalimbali nchini ili kuhudumia wananchi katika kudhibiti uhalifu. Katika Tarafa ya Nanjilinji kinajengwa kituo cha Polisi kitakachogharimu shilingi 67,700,000. Kituo hiki kiko kwenye hatua ya umaliziaji ambapo jumla ya shilingi 62,000,000 zimetumika. Wizara kupitia Jeshi la Polisi itatenga kiasi cha shilingi 5,700,000 ili kukamilisha ujenzi huo kama njia ya kuunga mkono juhudi za wananchi waliochangia ujenzi huo.

Mheshimiwa Spika, Serikali inashauri wananchi wa Tarafa za Kipatimu na Njinjo kutenga maeneo ya kujenga vituo vya polisi na kuanza ujenzi na Serikali itaunga mkono kama ilivyofanya katika Tarafa ya Nanjilinji.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kukifanyia ukarabati Kituo cha Polisi cha Nansio?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uchakavu wa Kituo cha Polisi Nansio kilichopo Ukerewe. Tathmini kwa ajili ya ukarabati imeshafanyika mwaka huu wa 2022 na kubaini kuwa kiasi cha shilingi 68,000,000 zinahitajika ili kugharamia ubadilishaji paa, dari, mfumo wa maji na maji taka, pamoja na kuziba nyufa, kurekebisha sakafu pamoja na kupaka rangi. Ukarabati huu utafanyika kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza: -

Je, kuna wahanga wangapi wa vitendo vya ukatili nchini kuanzia mwaka 2019 hadi 2022?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za matukio ya vitendo vya ukatili nchini vilivyoripotiwa kwenye Vituo vya Polisi kuanzia mwaka 2019 hadi Machi, 2022 ni 27,838 kwa mchanganuo ufuatao: -

Matukio ya kubaka ni 19,726; kulawiti ni 3,260 ambao kati ya hao wanaume ni 3,077 na wanawake ni 183; kuunguzwa kwa moto ni 198 kati ya hao wanaume ni 73 na wanawake ni 125; kutupa watoto wachanga ni 443 kati yao wanaume ni 177 na wanawake ni 266; kipigo ni 4,211 ambao kati ya hao wanaume ni 16 na wanawake ni 4,195.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya kesi zilizofikishwa Mahakamani ni 21,063 na watuhumiwa ambao wamehukumiwa 14,278. Mashauri mengine yako kwenye hatua mbalimbali za upelelezi pamoja na Mahakamani. Aidha, Serikali inaendela kuiasa jamii kutumia vema taasisi za familia kaya, jumuiya za kidini kuanzia ngazi za vitongoji, vijiji na mitaa ili kudhibiti vitendo vya ukatili katika jamii.
MHE. JERRY W. SILAA aliuliza: -

Je, ni Sheria gani inasimamia orodha ya wanaostahili kutumia ving’ora na vimulimuli kwa misafara ya Viongozi na Wananchi wa kawaida?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Usalama Barabarani Sura ya 168 ya mwaka 1973 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002, ndiyo sheria inayosimamia matumizi ya ving’ora na vimulimuli barabarani. Kifungu 39(b) kifungu kidogo cha (1) na (2) cha sheria, kinaelekeza matumizi ya ving’ora na vimulimuli barabarani ambayo ni kutoa ishara kwa watumiaji wengine wa barabara kuchukua tahadhari kuwa kuna dharura. Kifungu cha 54 kifungu kidogo cha (1) hadi cha (5) kinaeleza utaratibu na mazingira ya matumizi ya ving’ora na vimulimuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, magari yanayostahii kutumia ving’ora na vimulimuli kwa mujibu wa sheria ni magari ya polisi, zimamoto, magari ya wagonjwa (ambulance), magari ya vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na magari yaliyopata kibali maalumu kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na kutangazwa katika Gazeti la Serikali.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuunganisha mifumo ya Kitambulisho cha Mpiga Kura na Kitambulisho cha Taifa ili kuepusha usumbufu kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Askofu Josephat Mathias Gwajima, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuunganisha mifumo ya Kitambulisho cha Mpiga Kura na Kitambulisho cha Taifa ili kutumia Kitambulisho cha Taifa katika uchaguzi wa kawaida na ule wa kieletroniki (e- voting).

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi haya yatapunguza gharama kwa Serikali katika kuandikisha na kutengeneza daftari pamoja na kurahisisha usimamizi wa wapiga kura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano kati ya Taasisi hizi mbili yenye dhumuni la kuwezesha kanzidata ya NIDA kutumika katika katika zoezi la uboreshaji wa daftari la Wapiga Kura yameanza mwezi Machi, 2022. Mazungumzo ya awali kati ya wataalam wa taasisi zote mbili yenye nia ya kuunganisha mifumo hiyo miwili yamepangwa kufanyika kabla ya mwezi Mei, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matarajio ya Serikali ni kuona mifumo hiyo inaunganishwa ili kuwarahisishia wananchi kushiriki katika shughuli za uchaguzi na kuipunguzia Serikali gharama katika uandikishaji na uchapishaji wa vitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.(Makofi)
MHE. HAJI AMOUR HAJI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itashughulikia suala la mtambo wa kielektroniki ulioharibika kwa zaidi ya mwaka sasa na kusababisha mlundikano mkubwa wa hati za ukaazi katika Idara ya Uhamiaji Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haji Amour Haji Mbunge wa Pangawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwezi Januari, 2020 hadi Juni, 2020 mtambo wa kuchapisha kadi za vibali vya elektroniki vya hati za ukaazi (E-Permit) wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar ulisitishwa na kupelekea kadi za hati za ukaazi 139 kuchelewa kuchapishwa kwa sababu ya hitilafu ya mtambo wa kuchapia kadi za vibali vya hati za ukaazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, huduma za utolewaji wa hati za ukaazi ziliendelea kutolewa kwa wageni kwa kugongewa muhuri katika pasipoti ili kuthibitisha kuwepo kwao kihalali hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia Julai, 2020 huduma za utoaji wa hati za kielektroniki ziliendelea kutolewa ambapo hadi kufikia mwezi Machi, 2022 jumla ya vibali 799 vya hati za ukaazi vya kielektroniki vimetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kuruhusu Mabasi ya Abiria yanayopita Wilayani Sikonge kuendelea na safari badala ya kuyalazimisha kulala?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI, alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Mbogo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mabasi ya abiria yanayokwenda Mpanda Mkoa wa Katavi ambayo yanapita Wilaya ya Sikonge zaidi ya saa nne usiku hushauriwa kulala Sikonge kwa sabubu za kiusalama. Eneo hilo lina pori la hifadhi kuanzia Sikonge hadi Inyonga lenye urefu wa kilometa 161 na halina mtandao wa mawasiliano. Hivyo si salama kupita nyakati za usiku mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuepuka adha ya kutakiwa kulala Sikonge, wamililki wa mabasi ya abiria wanashauriwa kupanga safari zao ili wapite katika maeneo hayo yenye changamoto mapema zaidi. Mabasi hayo yanaweza kuomba kuanza safari zao hasa kutoka Dar es Salaam saa tisa au saa kumi Alfajiri na Serikali itaafiki maombi yao.
MHE. MWATUMU DAU HAJI aliuliza: -

Je, lini Serikali itaongeza gari lingine la polisi wilaya ya Kusini Unguja kwani gari moja lililopo halikidhi mahitaji?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwatumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi wilaya ya Kusini Unguja, katika mkoa wa kusini Unguja una magari manne ambayo yote ni mazima na yanatumika kutoa huduma katika eneo hilo. Magari hayo ni PT 4807 Ashok Leyland ambalo liko kituo cha Polisi Kizimkazi, PT 4808 Ashock Leyland ambalo liko Kituo cha Polisi Paje, PT 1906 Toyota Land Cruiser ambalo lipo Kituo cha Polisi Paje, PT 3860 Toyota Hilux Double Cabin ambalo liko kituo cha Polisi cha Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia bajeti yake ya mwaka wa fedha 2022/2023 imetoa kiasi cha fedha shilingi billioni 15 kwa ajili ya Jeshi la Polisi ili kununulia pikipiki pamoja na magari ambayo yamepangwa kugawiwa kwenye mikoa na wilaya zote nchini.
MHE. AGNESTA L. KAIZA aliuliza: -

Je, Serikali ipo tayari kuruhusu uraia pacha kwa Watanzania wenye uraia wa nchi nyingine?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimwa Agnesta Lambert Kaiza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uraia wa Tanzania unaongozwa na Sheria ya Uraia ya Tanzania Sura ya 357 Rejeo la mwaka 2002. Sheria hii inabainisha aina tatu za uraia wa Tanzania ambazo ni uraia wa kuzaliwa, uraia wa kurithi na uraia wa tajnisi.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Uraia tajwa hapo juu, Serikali hairuhusu uraia pacha kwa watu wazima isipokuwa kwa watoto wenye umri chini ya miaka kumi na nane ambao wanakuwa na uraia wa Tanzania na uraia wa nchi nyingine.
MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kubadili utaratibu wa malipo kwa wastaafu wa Jeshi la Polisi wa Zanzibar ili kuondoa usumbufu wanaoupata?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali utumishi wa Askari Polisi ulikuwa kwenye masharti ya pensheni na bakshishi. Askari ambaye hakuwepo kwenye masharti ya pensheni alifanya kazi kwa mkataba wa miaka 12 kwa kujaza mkataba wa kipindi cha kila baada ya miaka mitatu kumalizika. Kwa mujibu wa Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi Sura ya 322, askari kwa hiari yake mwenyewe baada ya mkataba alipaswa kufanya chaguo la ama kuendelea na utaratibu wa ajira ya mkataba na kwa malipo ya bakshishi ambao ukomo wake wa utumishi ni miaka 21 au kuingia kwenye utaratibu wa ajira ya malipo ya pensheni na kulipwa mafao ya uzeeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Jeshi la Polisi limefanya maboresho kwa kuondoa utaratibu wa mkataba wa miaka 12 na kuwa miaka sita pamoja na kuondoa chaguo. Na baada ya mkataba kumalizika askari wote wanaingia kwenye ajira ya kudumu yaani pensheni.
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH aliuliza: -

Je, lini Serikali italipa madeni ya fedha za kusafirishia mizigo kwa Askari Wastaafu?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi limeshafanya uhakiki wa madeni ya kusafirisha mizigo ya askari polisi wastaafu 624. Uhakiki huo unaonesha kuwa jumla ya fedha zinazohitajika kwa ajili ya kusafirisha mizigo ya askari polisi wastaafu ni shilingi 806,067,788.02. Madai hayo yatalipwa baada ya Wizara ya Fedha kukamilisha taratibu za kuhamishia fedha hizo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kukamilika. Ninakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga Vituo vya Polisi kwenye Kata za Mkiwa, Misughaa na Mungaa pamoja na nyumba za kuishi askari Singida Mashariki?

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inazo taarifa kuwa Kata za Mkiwa, Misughaa na Mungaa zimeshatenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya Polisi na nyumba za makazi ya askari. Serikali kupitia Jeshi la Polisi inasubiri kupata taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa vituo na nyumba hizo ili kuunga mkono kwenye ukamilishaji. Nakushukuru.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA aliuliza:-

Je, lini Kituo cha Polisi Bububu pamoja na nyumba za Askari vitafanyiwa ukarabati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Jimbo la Bububu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imepanga kukarabati Kituo cha Polisi cha Bububu kwa awamu. Kwa awamu ya kwanza Serikali inakarabati hanga la kuishi familia 18 za askari ambalo linagharimu shilingi 19,358,450 na kwa sasa umefikia katika hatua ya umaliziaji. Baada ya awamu hii, Serikali imepanga kutumia shilingi 46,000,000 kukarabati kituo hicho pamoja na nyumba za askari katika mwaka wa fedha 2024/2025, nakushukuru.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI aliuliza:-

Je, lini Serikali itafanya ukarabati wa nyumba za makazi ya polisi Moshi Manispaa?
NAIBU WAZIRI, MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini kwa ajili ya ukarabati wa nyumba 147 za makazi ya askari polisi zilizoko Manispaa ya Moshi imeonesha kuwa kiasi cha shilingi bilioni 3.6 zinahitajika. Fedha hizo zinatarajika kutengwa kwa awamu kuanzia kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2024/2025 ambapo ukarabati wa nyumba 15 unatarajiwa kuanza kutekelezwa, nakushukuru. (Makofi)
MHE. MBAROUK JUMA KHATIBU aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kujenga Kituo cha Polisi katika eneo ambalo linajengwa Bandari Kuu ya mizigo Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbarouk Juma Khatibu, Mbunge wa Jimbo la Bumbwini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Bandari ambayo imejenga bandari ya mizigo eneo la Manga Pwani – Zanzibar imetenga eneo na imeandaa michoro kwa ajili ya kujenga ofisi zitakazotumiwa na vyombo vya ulinzi na usalama kikiwemo kituo cha polisi, ninakushukuru.
MHE. GRACE V. TENDEGA K.n.y. MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza: -

Je, ni asilimia ngapi ya Watanzania wameandikishwa na kupatiwa Vitambulisho vya Taifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: =

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia Tarehe 31 Julai, 2023, jumla ya Watanzania 11,242,736 wamepewa vitambulisho, sawa na asilimia 55 ya lengo la kuwapatia wananchi 20,294,910 wanaostahili kupewa. Mpango wa Serikali ni kuwagawia vitambulisho Watanzania waliobaki ifikapo Machi, 2024, ninakushukuru.
MHE. OMAR ISSA KOMBO K.n.y. MHE. AMOUR KHAMIS MBAROUK aliuliza: -

Je, kwa nini Serikali imehamisha Kituo Kidogo cha Polisi Tumbe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amour Khamis Mbarouk, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, shughuli na huduma za Kituo cha Polisi Tumbe kilichopo Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, zimehamishwa toka Tumbe kwenda Kituo cha Polisi Konde. Sababu ya kufanya hivyo ni uchakavu wa jengo lililokuwa linatumika kama kituo cha polisi ambalo ni mali ya Shehia ya Tumbe Mashariki. Jengo hilo halifai tena kwa matumizi ya kazi za polisi. Eneo hilo pia ni finyu na limezingirwa na nyumba za makazi ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kutumia fursa hii kumshauri Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Micheweni kupata eneo kubwa zaidi lenye angalau ukubwa wa square meters 3,000 kwa ajili ya kujenga kituo cha polisi eneo hilo la Tumbe. Wizara kupitia Jeshi la Polisi itaunga mkono katika ujenzi wa kituo hicho kipya, ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati kwenye Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kibondo pamoja na nyumba za Askari Polisi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kibondo pamoja na nyumba za makazi ya Maofisa na Askari ni chakavu. Tathmini ya uchakavu kwa ajili ya kufanya ukarabati imefanyika na kiasi cha Sh.28,914,250/= kinahitajika kwa ajili ya kukarabati Kituo cha Polisi na Sh.109,288,000/= zinahitajika kwa ajili ya ukarabati wa nyumba nane za makazi ya Maofisa na Askari Polisi. Kulingana na hali ya upatikanaji wa fedha, Serikali imepanga kutekeleza ukarabati huo katika mwaka wa fedha 2024/2025, nakushukuru.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za ujenzi wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Liwale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Liwale imetoa eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 10,000 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Polisi pamoja na nyumba za makazi ya askari. Tathmini ya makadirio na michoro kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi, daraja B umeshafanyika na kiasi cha Sh.768,024,734/= kinahitajika. Fedha hizo zitatolewa kwenye Mfuko wa Tuzo na Tozo katika mwaka wa fedha 2023/2024, nakushukuru.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi katika Mji Mdogo wa Ngaramtoni?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mollel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Polisi haina eneo lililotengwa na Halmashauri kwa ajili ya kujenga Kituo cha Polisi na nyumba za makazi ya Askari. Tunazo taarifa kwamba Mamlaka ya Mji Mdogo wa Ngaramtoni inaendelea na mchakato kwa Halmashauri ya Wilaya ya Arumeru kupata eneo na kutenga kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za taasisi za umma ikiwemo Kituo cha Polisi na nyumba za makazi ya Askari. Pindi eneo hilo litakapopatikana Wizara itatenga fedha za ujenzi wa kituo na nyumba za makazi ya Askari kupitia Jeshi la Polisi, ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza:-

Je, upi mpango wa kuboresha Vituo vya Polisi Busanda hususani Kituo cha Katoro na Chigunda?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama maandalizi ya kuboresha vituo vya Katoro na Chigunda, tathmini kwa ajili ya ukarabati na uboreshaji wa mazingira ya vituo hivyo imeshafanyika na kubaini kuwa kiasi cha shilingi 37,265,000 zinahitajika. Fedha hizo tunatarajia kuzitenga kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka 2024/2025 ili kugharamia ukarabati wake.