Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ritta Enespher Kabati (84 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha , Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa ili tuweze kuujadili.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo naomba Serikali iweze kunipatia ufafanuzi wake:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza viwanda; ni imani yangu kuwa kama viwanda vitaimarishwa nchini, Serikali itaongeza pato la Taifa na tutaongeza ajira kwa vijana wetu nchini.
Ningeomba kujua, nchi yetu ilikuwa na viwanda vingi sana, ambavyo vingi vyao vilibinafisishwa na wawekezaji wengine wamebadilisha matumizi ya viwanda hivyo. Je, nini mpango wa Serikali kwa viwanda hivyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, tulikuwa na kiwanda cha kuchonga almas cha Tancut Iringa, ambacho kilikuwa kinatumia malighafi za ndani, lakini leo hii almas yetu inapelekwa nje kuchongwa. Tungependa Serikali iweke Mpango wa wazi unaoeleza jinsi ya kuanzisha viwanda vitakavyotumia kununua bidhaa za ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, miundombinu ya barabara; ningependa kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha barabara zote za kiuchumi zinapitika wakati wote ili kuweza kuchukua mazao na malighafi kama Mgololo kilichopo Iringa, hiyo ingejengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Iringa ni kati ya Mikoa ya kiuchumi. Kwa mfano, tunalima mahindi kwa wingi, vitunguu, nyanya, chai na tuna msitu mkubwa sana wa miti, lakini barabara zake zote zinazokwenda kwenye maeneo hayo zina hali mbaya sana! Ningependa jambo hili, Serikali itoe kipaumbele. Pia zipo barabara kama ile inayokwenda kwenye Mbuga ya Wanyama ya Ruaha National Park iwekewe lami ili tupate Watalii wengi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, umeme; Viwanda vitakapoanzishwa vitahitaji umeme wa uhakika, umeme usio katikakatika kama tulionao hivi sasa na kuwepo umeme, mijini na vijijini ambao ni wa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nne, kilimo; kwa kuwa nchi yetu, wananchi wake asilimia kubwa sana wanategemea kilimo na tunategemea Serikali yetu iweke mpango mahususi kwa ajili ya kusaidia wakulima. Wakulima wapatiwe elimu ili walime kilimo cha kisasa na chenye tija na kitakachoweza kusaidia malighafi katika viwanda vyetu pamoja na kupatiwa mikopo katika Benki yetu ya Kilimo. Je, ni kwa nini Serikali isifungue Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Dodoma ili Benki hii iweze kufikiwa na mikoa yote kuliko ilivyo sasa, Benki hii ipo Dar es Salaam tu?
Mheshimiwa Naibu Spika, tano, uimarishaji wa miradi ya vyanzo vya mapato; Serikali iwe na mpango madhubuti wa kumalizia miradi ambayo imechukua muda mrefu sana, ambayo inaweza kuongeza pato la Taifa kwa sababu tumekuwa tukianzisha miradi mipya wakati miradi ya zamani inasuasua!
Mheshimiwa Naibu Spika, sita, ujenzi wa reli na viwanja vya ndege; bila Serikali kutoa kipaumbele katika ujenzi wa reli bado tutaendelea kusuasua sana katika ukuzaji wa pato letu la Taifa. Reli itaponya hata barabara zetu nchini na kupunguza hata bei ya bidhaa. Pia Serikali ieleze wazi mpango hata kuhakikisha viwanja vyetu vya ndege vinajengwa ili viweze kusaidia kukuza pato la Taifa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha Hotuba yao ili tuweze kuijadili. Yapo mambo ambayo naomba kupata ufafanuzi na kuishauri Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Maboresho ya maabara katika shule zetu. Katika Mkoa wetu wa Iringa kuna shule nyingi sana za sekondari bado maabara zake hazijaweza kuboreshwa vizuri ili kuweza kumsaidia mtoto anayesoma masomo ya sayansi. Pamoja na kutokamilika kwa majengo kwa baadhi ya shule, lakini hata vifaa vya kutumia katika maabara kwa baadhi ya shule bado havikidhi haja. Vile vile pamoja na Sera ya Serikali kupeleka umeme wa REA katika taasisi kama shule zetu za sekondari na vyuo, bado hakuna umeme. Sasa tunategemea hawa watoto wakifanya mtihani kweli watafaulu kwa mtindo huu, tutapata kweli wataalam wa sayansi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule kongwe na maboresho ya shule maalum. Katika Mkoa wetu wa Iringa tunazo zile shule kongwe za sekondari kama Shule ya Lugalo, Shule ya Tosamaganga, Shule ya Malangali, hizi shule zinahitaji ukarabati wa hali ya juu.
Ningeomba sasa Serikali itoe kipaumbele katika ukarabati wa majengo ya shule hizi tu. Shule ya Sekondari Lugalo sasa hivi ni shule maalum, inachukua watoto wanaofundishwa elimu maalum, kama watoto wenye ulemavu wa ngozi, watoto viziwi, watoto wasioona, lakini inasikitisha sana kuona shule hii hawa wenye elimu maalum hawana vifaa vya kujifunzia. Je, ni utaratibu gani unatumika ili hawa vijana waweze kupata vifaa vya Walimu wao kuwafundishia na vifaa vya kujifunzia?
Mheshimiwa Mwenyekiti, maboresho ya mitaala kwa Walimu. Serikali imekuwa ikibadilisha mitaala lakini Walimu hawapati semina au elimu kwa ajili ya kuweza kuielewa hiyo mitaala ili waweze sasa kufundisha kwa watoto. Hivyo, Serikali kama inabadili mitaala iende sambamba na kuwafundisha Walimu hao hiyo mitaala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, madeni ya wazabuni. Naomba Wizara ifanye utaratibu wa kulipa madeni yote ya wazabuni. Wazabuni wanapata shida kwa muda mrefu sasa. Ningeomba Waziri anapojibu atueleze mkakati wa Serikali wa kulipa madeni ya wazabuni, yamekuwa ni ya muda mrefu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia mada iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimwa Rais alipokuwa anapokea ile ripoti ya makinikia ya pili aliomba sisi Watanzania tumuombee, hasa na mimi nikaona nitayarishe vifungu ni nukuu kidogo hapa katika Bunge letu ili wale ambao wanakuwa hawasomi Biblia waweze kusoma na naomba nisome Timotheo wa Pili Mlango wa Kwanza mpaka wa Tatu; “Basi kabla ya mambo yote wataka dua sala, maombezi na shukrani zifanyike kwa ajili ya Wafalme na wote wenye mamlaka ili tuishi maisha ya utulivu na amani.”

Lakini ukisoma Waibrania 13 mpaka 17 inasema; “Watiini viongozi wenu na kuwa wanyenyekevu maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu kama watu watakaotoa hesabu ili kwamba wafanye kazi yao kwa furaha na kwa manufaa yenu.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Magufuli ni zawadi kwa Watanzania ni Mussa wa Watanzania kwa vile Mungu alivyosikia kilio cha watu wa Taifa la Israel kuwakomboa toka utumwani na kuwapeleka Kanani vivyo hiyo Mungu amesikia kilio cha Watanzania wanyonge amemleta Rais Magufuli ili awe mkombozi wa kututoa katika utumwa, umaskini na kutupeleka katika neema kwa kudhibiti wizi wa madini na rasilimali za nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nitumie fursa hii sasa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika nchi yetu na niombe Watanzanila bila kujali itikadi zetu tuunge mkono kwa yote anayo yafanya kwa ajili ya Taifa letu. Nawapongeza Watanzania wote waliomuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu na hatua wanazozichukua kukabiliana na upotevu wa mapato ya Serikali katika sekta ya madini, nawapongeza Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa azimio lao ambalo walilitoa juzi kuunga mkono juhudi hizi za Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kumpongeza Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri katika Ofisi yake Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu wake Mheshimiwa Mavunde kwa kuaamua kuupatia heshima Mkoa wetu wa Iringa kuja kuzindua mafunzo ya ufundi kwa vijana wetu katika Chuo cha Don Bosco; mafunzo ambayo yatawanufaisha vijana karibu 3,440 na yataendelea kwa nchi nzima tena bure kabisa. Vijana 1,000 Mwanza, vijana 1,000 Morogoro, vijana 2,000 Dar es Salaam na vijana 4,000 ambao wamekuwa wakifanyakazi bila kupata mafunzo watapata vyeti vyao. Kwa hiyo, ni jambo jema ambalo Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inatakiwa iungwe mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeza sasa katika madaa nimpongeze Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mpango, Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Kijaji na watendaji wote wa Wizara kwa hotuba yake ya bajeti nzuri na yenye mashiko, na ambayo imejali watu wote wakulima, wafanyakazi, wote imewajali kwa kweli. Lakini naomba kabla sijaanza kuchangia kabisa na mimi ni nukuu katika hotuba ya msemaji wa Kambi ya Upinzani ukurasa wa tatu maneno ya hayati Nelson Mandela “No easy walk to freedom.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie wenzangu Wapinzani kuwa nchi hii ilikwisha pata uhuru kwa njia ya amani na utulivu. Sasa sijui wenzetu wanapigania uhuru wa nchi gani maana nchi yetu ilikwisha kombolewa kutoka kwa wakoloni kwa jitihada za TANU na sasa hivi ndio CCM na hao hao NAC tuliwasaidia Watanzania kupata uhuru kutoka kwa makaburu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali katika bajeti hii kwa kuwatambua rasmi wafanyabishara wadogo wadogo wasio rasmi na wanafanya biashara katika maeneo yasiyo rasmi kama mama lishe, wauza mitumba wadogo wadogo, wauza mazao ya kilimo kwa kuwapatia vitambulisho maalum kazi wanazozifanya. Lakini nilitaka kujua je kuhusiana na vijana wa bodaboda na wenyewe wako maana yake kwenye kitabu kile hawajasema maanake nao wamekuwa wakitoa kodi naomba na wenyewe labda watakapokuwa wanajibu watuambie kama na bodaboda na wenyewe wapo.

Pia nilikuwa naomba Halmashauri zetu ziandae sasa mazingira rafiki kwa hawa wafanyabiashara waweke miundombinu rafiki, kuwepo na maji, kuwepo na umeme na waangalie sehemu ambazo hawa wanaweza wakafanya biashara zao na wakapata faida. Kwa sababu utakuta Halmashauri zetu zimekuwa zikitenga maeneo ambayo sio rafiki na biashara na kuwasababisha vijana wetu kushindwa kufanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi pia niungane na wote waliochangia kuhusiana na tozo ile ya shilingi 40 katika mafuta mimi nilikuwa naomba kweli ipelekwe moja kwa moja katika mradi wa maji. Kwa sababu maji vijijini ili dhamira ya kumtua ndoo kichwani mwanamke iweze kutimia kwa sababu ukiangalia katika Mkoa wetu utakuta miradi hii ya maji mingi sana imekwama, visima vingi vimechimbwa lakini havitoi maji na vilevile unakuta kuna vyanzo vya maji vingine ambavyo bado sio salama, kwa hiyo, kuna maziwa na mito mingi lakini bado hatujaweza kupatiwa maji vizuri katika Mkoa wa Iringa maji vijijini ni tatizo kubwa sana. kwa hiyo nilikuwa naomba ile tozo iende moja kwa moja kwenye maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuchangia kuhusiana na hoja hii nafikili tunaelekea katika uchumi wa viwanda lakini bila kutoa kipaumbele katika barabara zetu za kiuchumi bado tunapatashida sana, kwa sababu ndizo ambazo zenye malighagfi, utakuta katika Mkoa wetu wa Iringa barabara nyingi sana za kiuchumi hazina lami. Kwa hiyo, utaona kwamba zile malighafi wakati wa mvua malori yanakuwa yanakwama ukienda kule Mufindi, Kilolo unakuta kwamba yale malori yanakwama kule kwa hiyo mimi nilikuwa naomba Serikali itoe kipaumbele ihakikishe kwamba barabara zote za kiuchumi zinawekewa lami ili kusaidia hata kukuza uchumi huu wa viwanda kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipochangia mara ya kwanza nilichangia kuhusiana na Benki ya Wanawake; kwa kweli hii Benki ya Wanawake sisi kwa Wanawake ni mkombozi na nilisema kwamba imeshafungua baadhi ya madirisha katika baadhi ya Mikoa ambayo sio ming, ningeomba Serikali kwa kweli iangalie kwa karibu ili iweze kuipatia ile pesa ambayo ruzuku ambayo ilikuwa Serikali imeamua kuwapatia ili Wanawake wote wafaidike kwa sababu Wanawake wengi sana walikuwa wanaaibishwa, ndoa nyingi sana zimevunjika kwa sababu wanaenda kuchukua kwenye taasisi za fedha nyingine ambazo zinawafanya wanawake wanadhalilika wanawake ndoa zimevunjika, wanauziwa mali zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naamini kwamba kwa sababu Serikali na tulikaa kwa pamoja na tukaamua kwamba Benki ya Wanawake iwanufaishe Wanawake wote basi Serikali iweze kutoa pesa ambayo ruzuku ilikuwa imeahidi kwamba ingeweza kuwa inatoa kila bajeti ili madirisha mengi sana yaweze kufunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu kinu chetu cha Iringa pale National Milling, nililisema siku ile kwenye swali, kile kinu tuna imani kwamba NSSF walisema kwamba wangetusaidia ili kile kinu kiweze kusaidia wakulima wa Iringa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kwa kweli hili nalo lizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme kwamba makinikia yetu sisi Iringa ni vinyungu, utaona Wabunge wengi sana wamechangia hapa wakizungumzia kuhusu vinyungu. Vinyungu ndio mkombozi wa wana Iringa sasa nisipozungumza sasa hivi wanawake wote wanashindwa, maana yake ilikuwa mwaka mzima unalima, mwaka mzima unafanya biashara kupitia vinyungu vile, hata mimi mwenyewe nimesomeshwa kwa vinyungu. (Makofi)

Kwa hiyo, mimi naomba Serikali iangalie upya hili suala la vinyungu maana yake hata kwa Wasukuma kule wanaita majaruba maana mimi nimeolewa na Wasukuma wanaita majaruba kwa hiyo kila nchi wanaita kwa majina yao, kwa hiyo ningeomba hivi viangaliwe upya ili wananchi waendelee kutumia maana yake naona Wabunge wengi wa Iringa pia wamezungumzia kwa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza haya kwa kweli kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu na niseme kwamba Waziri wa Fedha kanyaga twende, fanya kazi, tunajua kwamba tunakuamini, wewe ni Waziri ambaye umekuwa ukitusaidia sana, kwa hiyo, endelea na Naibu wako, fanyeni kazi leteni bajeti na niombe sasa pesa zifike kwa wakati kwenye Halmashauri zetu ili ile miradi ya muda mrefu iweze kumalizika kwa wakati kwa sababu tumekuwa na miradi mingi ya muda mrefu ambayo sasa mkichelewesha pesa gharama inakuwa inaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo naomba nikushukuru na ninaunga mkono hoja kwa asilimia 150.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti iliyoko mezani kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze na kuipongeza Serikali hii ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa sana ambayo ameifanya kwa kweli katika nchi yetu na hata imefanya baadhi ya viongozi wetu akiwepo Mheshimiwa Lowassa kurudi CCM, baadhi ya Wabunge wengine wote kurudi CCM na viongozi mbalimbali baada ya kuona kazi nzuri sana na mno inayofanywa na Chama chetu cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi yake nzuri. Kwa kweli, amefanya kazi nzuri sana, ametembea karibu nchi nzima kuhakikisha kwamba miradi inakwenda. Pia nawapongeza Mawaziri waliopo katika Ofisi ya Waziri Mkuu; Mheshimiwa Jenista Mhagama, Mheshimiwa Ikupa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa kuongeza tena kasi katika ofisi yake kwenye suala la uwekezaji. Ninaamini kabisa uwekezaji sasa unaenda kuinua nchi yetu. Bila kuwekeza, sidhani kama nchi yetu itaweza kusikika hata katika viwanda au katika nyanja zozote. Bila kuwekeza, kuleta wawekezaji, kuweka vivutio vingi na kutoa changamoto nyingi ambazo kwa kweli tulikuwa tunaona kama ni kero sana katika nchi yetu, nchi hii haiwezi kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri kwamba Mheshimiwa Jenista sasa apewe wataalam na ofisi ambayo itasaidia sasa kuondoa ule urasimu ambao ulikuwepo kwa wawekezaji wetu ili waweze sasa kuwekeza na nchi yetu iweze kuongeza ajira na kipato kikubwa kabisa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nipongeze sana mambo makubwa yanayofanyika katika Mkoa wetu wa Iringa. Ukarabati wa Kiwanja cha Nduli, kwa kweli Wana- Iringa tunasema Kamwene. Kazi ile ni nzuri sana na mpaka sasa hivi ukarabati ule tarehe 29 nawakaribisha wote, ndege kubwa Bombadier inatua pale Iringa. Kwa hiyo, niwaombe muionje siku hiyo, twende tukatue pale hata Naibu Spika ili mwone kazi na kasi kubwa kabisa inayofanywa na nchi yetu ikiongozwa na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, Iringa ni kitovu cha utalii, sasa ukarabati ule uende sambamba na ukarabati wa kiwango cha lami, ile barabara inayokwenda mbuga za wanyama Ruaha Nationa Park kwa sababu, ni mbuga ya pili. Tunaamini kama itajengwa kwa kiwango cha lami, sasa utalii utaongezeka, uchumi wetu wa Iringa na uchumi wa nchi hii kutumia utalii tutaongeza hata watalii wengi sana watakuja, hata wananchi watajiajiri kwa kupitia utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naiomba Serikali yangu, wale wananchi waliopisha ukarabati ule, basi wapewe fidia zao mapema kabisa. Vilevile uzio ujengwe kwa sababu kuna wanyama wanazunguka, ili kuhakikisha kwamba mambo ni motomoto Iringa. Iringa siyo ile ya wakati ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nizungumzie kuhusu utafiti. Kwa kweli nchi hii haitaendelea bila kufanya tafiti mbalimbali, kwa sababu, tunavyo vituo vingi sana vya utafiti; TARIRI, COSTECH, NIMRI na NBC. Hivi vituo vina hali mbaya mno. Sasa tutaendeleaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, bila kuboresha mambo ya utafiti, bila kutenga pesa ya utafiki katika hivi vituo ili tafiti mbalimbali katika nchi hii ziweze kufanyika, hatutakwenda. Nchi za wenzetu zinaendelea kwa sababu wanafanya tafiti za kutosha. Tunaona tunapata pesa za kigeni, lakini wao wanalenga tunataka kufanya tafiti tulani. Nchi yetu bado hatujajipanga kuweka pesa ya kutosha kwenye utafiti. Unaona karibu 90% inaenda kwenye ya mbegu. Asilimia 90 tunaagiza mbegu kutoka nje wakati tunacho Kituo cha Utafiti cha Mbegu nzuri, nasi tumekwenda, wanashindwa tu kupata pesa. Kuna changamoto kubwa sana kwenye vituo hivi vya tafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yetu kwa kweli sasa ione umuhimu mkubwa kabisa wa kuhakikisha tunatenga fedha za utafiti. Kwa tulishasema katika Mpango wa Maendeleo kwamba 1% ya bajeti tutenge kwa ajili ya tafiti mbalimbali hapa nchini. Kwa hiyo, naomba hii iwe ni lazima itengwe ili tufanye utafiti wa kutosha ili uchumi wa viwanda uende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nielezee kitu kingine kuhusu barabara zetu za kiuchumi. Barabara za kiuchumi kwa kweli naomba zipatiwe kipaumbele cha kutosha. Kwa sababu barabara nyingi sana za Mkoa wetu wa Iringa ambazo ndiyo uchumi mkubwa; na nafikiri tunaenda kwenye viwanda na kule ndiyo kuna malighafi za kutosha, bado sasa hivi hazipitiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu mfano mmoja, kwa sababu najua nitakuja kuchangia kwenye mambo ya barabara; utakuta pale Mufindi kuna Barabara ile ya Mtirili – Ifwagi – Mdabulo – Ihanu – Mpanga TAZARA mpaka Mlimba huko kwenda kule kwa Mheshimiwa Susan Kiwanga. Hii barabara ni muhimu sana, lakini hapa ninapozungumza sasa hivi ile barabara haipitiki kabisa. Malori yamekwama, wananchi hawafanyi shughuli zozote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko barabara nyingi sana za Iringa ambazo kwa kweli ni za kiuchumi kabisa ambazo hazipitiki. Naomba hizi ziangaliwe na ikiwezekana tuzijenge kwa kiwango ambacho magari yaweze kupita yasilale barabarani, maana uchumi ndiyo unazidi kuharibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho nilitaka kuzungumzia pia kuhusiana na tozo katika viwanda vyetu, Mheshimiwa hizi tozo zimekuwa nyingi. Tumekuwa tukiuliza sana maswali hapa Bungeni, tozo zimekuwa nyingi mpaka wakati mwingine zinafika hata 28 kwenye viwanda vyetu. Sasa tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, lakini viwanda vinakufa kabla hata havijaanza kwa sababu, watu wakifikiria tozo nyingi sana karibu 28. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika usindikaji wa maziwa, nakipongeza sana kiwanda chetu cha ASAS pale Iringa, kinafanya kazi nzuri, kimetoa ajira nyingi sana, lakini tozo zimekuwa shida. Unakuta kwamba hata zile flavour za maziwa kila flavour inalipiwa. Sasa ifike sehemu jamani Serikali iangalie. Kwanza tusaidie viwanda vyetu vikue, kwa sababu viwanda vikikua, tukipata ajira nyingi, pato litaongezeka kwa kiasi kikubwa na hapo ndiyo tutakuta kweli kazi inakwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tulikuwa tumeenda kwenye ziara, kwa kweli wamempongeza sana Mheshimiwa Rais. Ziara yetu ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, tumepata pongezi nyingi sana kwa wananchi, lakini kuna changamoto ambazo zipo kwa mfano kwenye miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta katika miradi ya maji kwanza vibali vya kutoa vile vifaa kwa ajili ya kufanyia kazi havitoki kwa wakati. Kwa mfano, tulienda kwenye mradi ule wa maji Arusha. Ule mradi tayari maji yameshatobolewa pale Moshi, lakini sasa ili waanze kufanya ile kazi, bado hawajapewa vibali. Mizigo iko bandarini imekaa karibu wanasema kwamba ni miezi mitatu sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi, hii miradi ni ya kwetu, Serikali ya kwetu, hebu wekeni mpango mzuri kuhakikisha kwamba vitu vikija kwa mfano labda hawa wenzetu ambao wamekata huu ukandarasi, basi vifaa vyao vitolewe haraka sana bandarini ili iweze kusaidia miradi iende kwa haraka ili gharama za kutengeneza hii miradi ziwe kwa kiasi cha chini. Tunapochelewesha hii miradi kwa ajili tu ya kuchelewesha vifaa bandarini sidhani kama inaleta picha nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walisema pia vibali vya kazi vya wataalamu wao vinachelewa kutoka. Kwa hiyo, hilo nalo liangaliwe kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nisisahau, sisi ni walemavu watarajiwa. Nizungumzie watu wenye ulemavu. Mheshimiwa Ikupa nakupongeza sana, umefanya kazi nzuri sana, mpaka Iringa umefika, lakini kwa kweli kuna tatizo ambalo liko. Watoto wenye ulemavu wanapoenda kwenye hizi shule, zamani walikuwa wanapatiwa nauli. Sasa matokeo yake watoto wanabaki kwenye mashule hawarudi kwa wazazi wao. Wazazi wao wengi hawana uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iweke utaratibu wa kuwasaidia hawa watoto wenye ulemavu ili mara wanapofunga shule, basi warudi kwa wazazi wao. Hili ni tatizo kubwa, naomba Serikali iliangalie kwa umuhimu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Kamal Steel, kwa kweli, namshukuru Mheshimiwa Ikupa, alitualika tukaenda kwenye kiwanda cha Kamal. Amekuwa akisaidia sana, ameweka kiwanda kwa ajili ya kutengeneza viungo. Kama watu hawafahamu hapa, basi Kamal anafanya hiyo kazi na kwa kweli, ametoa viungo vingi sana vya bandia; na hata Mkoa wangu wa Iringa wameguswa, kwa sababu, pale tuna karibu watu wanaohitaji kama 100. Kwa hiyo, ameshatoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Mengi naye ametoa mchango, amewapatia mtaji watu wenye ulemavu waliopatiwa na Kamal shilingi laki mbili, mbili. Kwa hiyo, Mr. Mengi pia tunamshukuru kwa kuwasaidia watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, naomba pia nikupongeze, lakini niipongeze Tanzania yetu kwa michezo. Sasa hivi tuko mbali sana kimichezo na tupongeze hili kombe la AFCON kwamba angalau na sisi sasa tuko juu sana kimichezo. Tuendelee kusaidiana, tuendelee kushirikiana na kuhakikisha kwamba nchi yetu inapiga hatua kubwa kabisa katika michezo.

Mheshimiwa Spika, nina imani kabisa nchi hii tutaanza kutengeneza vipaji kwa watoto wetu, tutapata nchi ambayo itakuwa inatangazika kimichezo. Nafikiri kimichezo tunaweza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga. Naamini hutakosa kwenye mchango wa kuwachangia Yanga, maana umesisitiza watu tuchangie timu. Kwa hiyo, utaenda kuchangia Yanga. (Kicheko)

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo. Yanga unajua rangi zake ndiyo zitanifanya na mimi pia nichangie, lakini…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa. (Makofi/ Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu sana jioni hii. Kwanza kabisa naomba nimtangulize sana Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya kwa kuboresha Wizara ya Afya. Kwa kweli mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, Mheshimiwa Rais toka amechaguliwa ameweza kufanya kazi kubwa sana na hii kazi inaonekana hata huko vijijini kote anakokwenda pongezi nyingi amekuwa akizipata. Kwa hiyo kwa kweli tumpongeze na tupongeze Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuwachagua hawa Mawaziri, hajafanya kosa, dada yetu Mheshimiwa Ummy anafanya kazi nzuri sana. Hii Wizara nakumbuka kuna siku moja mtu mmoja alisema kwamba huyu dada anafanya kazi kama mwanaume, nikasema hapana, wanawake tunapiga kazi sio kwamba lazima awe mwanaume. Kwa hiyo dada Ummy anatutendea haki sisi wanawake wote. Vile vile Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Naibu Waziri pia kwa kweli anajituma, wakati wowote yuko tayari tukimwita anaitika na amekuwa anatusaidia kazi nyingi sana ambazo anatufanyia. Niwapongeze sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze Makatibu Wakuu, tena yuko mwanamke kwenye Wizara hii, hiyo ndio inahakikisha kwamba wanawake wanaweza, wachape mzigo, waoneshe kwamba sisi wanawake tukipewa kazi tunafanya kweli kweli, niwapongeze na watendaji wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali kwanza kabisa kwa kutenga pesa kwa ajili ya hospitali za wilaya 67, hospitali za mikoa nane, vituo vya afya 332 nchini na sisi katika mkoa wetu tuliweza kupata bilioni 4.5 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya ambazo kwa kweli tunashukuru Hospitali ya Kilolo, wakati wowote Mheshimiwa Rais atakuja kuizindua tunashukuru sana. Vilevile tumepewa pesa kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Mufindi na Hospitali ya Iringa DC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, hili ni ombi maalum tunayo Hospitali ya Frelimo ambayo yenyewe siyo inajengwa tayari ishajengwa kuanzia 2008 imeanza kufanya kazi. Sasa niombe kwa kweli Serikali ifanye utaratibu, hospitali ambazo tayari zinafanya kazi zina upungufu kwa mfano ile ya Frelimo ni kujengewa tu wodi za akinamama, akinababa na watoto ili kupunguza msongamano mkubwa kabisa uliopo katika hospitali ya mkoa. Kwa hiyo wangekuwa wanatoa kipaumbele kwa hospitali ambazo tayari zinafanya kazi na zinaweza kupunguza msongamano kwenye hospitali zetu za mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia Serikali iboreshe sasa vituo vya afya ambavyo vimeshajengwa ili kupunguza vifo vya akinamama na watoto kwa sababu kujenga ni kitu kingine, lakini tusipoboresha bado tatizo la vifo litabaki kuwa pale pale. Sasa niombe vifaa tiba vipelekwe, manesi wapelekwe ili kuhakikisha kwamba vituo vyote vinapatiwa pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sasa hospitali yetu ya mkoa. Hospitali yetu ya Mkoa ina changamoto nyingi sana; ya kwanza, Madaktari Bingwa wa Upasuaji wote hawapo, wameondolewa, wananchi wanapata shida mno, mno. Sasa hivi mgonjwa akitaka kufanya upasuaji, aidha apelekwe Muhimbili au aletwe Dodoma kwenye hospitali yetu ya Benjamini Mkapa. Bado kuna tatizo kubwa sana la magari, ambulance tuliyonayo imepewa jina la Ummy Mwalimu ambulance, ambayo kwa kweli kwanza ni ya petroli lakini imekuwa ndio hiyo hiyo moja nyingine zote ni mbovu, aidha wale Madaktari waweze kuchukua katika vituo vya afya na vituo vya afya bado vinakosa ambulance. Kwa hiyo nimwomba Mheshimiwa dada Ummy kwa heshima na taadhima kwanza kabisa aje pale Iringa atembelee hospitali yetu au Naibu azungumze na wafanyakazi walioko pale na Madaktari ili kwa kweli awape hata moyo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna upungufu wa watumishi, kuna upungufu wa Manesi, kuna upungufu pia wa nyumba na sio upungufu hakujawahi kujengwa nyumba za Madaktari kutokana na ufinyu wa eneo. Sasa niombe kabisa tufanye utaratibu wa kuhakikisha kwamba Madaktari wetu wanapatiwa nyumba kwa sababu hata call allowances zile zimekuwa ni shida mno kupatiwa pamoja na kuwa hawana nyumba, wanapokwenda kutibu wagonjwa usiku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona changamoto kubwa zilizopo katika hospitali zetu kwanza kabisa kukosekana kwa hizi mashine wagonjwa wanakufa mno kwa sababu ugonjwa wanaotibiwa wanakuwa hawaujui. Madaktari sasa wana- guess aidha huyu mtu anaweza akawa anaumwa homa au akiwa na homa pengine ana mafua au malaria. Sasa ni vizuri pengine kutokana na changamoto hii ya vifaa tungefanya hata miradi ile ya PPP ili waweze kufunga katika hospitali zetu, ni bora tulipie hiyo huduma kuliko kwenda kuitafuta hiyo huduma Muhimbili au kuja Dodoma. Kwa sababu ukienda Muhimbili bado utatumia gharama kubwa, lakini tukipata wawekezaji wakawekeza katika hospitali zetu itatusaidia, wagonjwa watatibiwa magonjwa ambayo kwa kweli yatasaidia kwamba watakuwa wanajua anachotibiwa mgonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Taasisi ya Saratani Ocean Road, Hospitali ya Benjamini Mkapa, kwa kweli hizi hospitali hata katika hotuba yake ametueleza kwamba zimefanya kazi kubwa kweli kweli, badala ya wagonjwa kupeleka nje ya nchi sasa hivi wanatibiwa hapa nchini. Hii ni kazi kubwa ya Chama hiki cha Mapinduzi na Rais wetu na Serikali hii kuhakikisha kwamba wananchi wanatibiwa hapa nchini. Hata hivyo, kuna changamoto, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize vizuri, wanapokwenda kutibiwa kwenye hizo hospitali, wanavyosubiri sasa tiba hizo labda kufanyiwa mionzi ya kansa au figo hawana pa kukaa, wamekuwa wakipata shida mno. Niombe sasa kama kuna uwezekano ufanywe utaratibu, watengenezewe maeneo maalum ya kuhakikisha kwamba wakati wanasubiria basi wanakaa pale, kwa sababu tumekuwa tukifanya michango kwa wagonjwa ambao wamekuwa wakitoka nje kwenda kusubiri hayo matibabu, kwa kweli hili naliomba liangaliwe kwa hali ya juu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwapongeze pia MSD, wanafanya kazi nzuri mno ya kusambaza dawa, nakumbuka kipindi kilichopita kila aliyekuwa anachangia alikuwa anasema upungufu wa madawa, lakini MSD sasa hivi inafanya kazi nzuri mno hata katika Mkoa wetu wa Iringa wamekuwa wakisambaza dawa, nimefanya ziara nimekuta wanafanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo niwaombe waendelee kufanya kazi hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu Bima ya Afya; nipongeze Bima ya Afya kwa Wote, kwa kweli huu mpango najua utachukua muda mrefu, lakini uwepo mchakato na wenzangu wamelizungumzia sana, uwepo mchakato wa haraka kuhakikisha wale ambao hawana Bima ya Afya sasa hivi wanakufa, kuna wengine ambao hawatibiwi, tufanye mchakato kwa sababu najua walio wengi na ndio wanyonge na Serikali hii inawajali wanyonge, sasa tuhakikishe hawa wanyonge wetu ambao hawana bima za afya tuwawekee utaratibu mzuri wa kuwatibu ili waweze kutibiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie huduma ya afya kwa watu wenye ulemavu; Mheshimiwa Ummy alishakuja kujionea kwenye kongamano la watu wenye ulemavu kwa Ikupa Trust Fund. Nami pia ni Mjumbe katika Kamati ya Watu Wenye Ulemavu, hawa watu wanapata shida sana kutokuwa na mkalimali wa kuwasaidia wakati wanaenda kwa Daktari. Sasa je, Serikali inawasaidiaje? Kuna mmoja alisema kwamba alipoteza mpaka mtoto wake, yeye ni kipofu lakini ameenda kujifungua mtoto kabadilishiwa mtoto, sasa wawekewe utaratibu mzuri kuhakikisha Watu Wenye Ulemavu nao wanatendewa haki katika matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie dawa za uti wa mgongo, ni ghali mno, watu wengi sana wanakufa mimi niliona, waweke utaratibu dawa hizi zipunguzwe bei ili watu waweze kutibiwa, zinaua watu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Bima ya Wazee na Watu Wenye Ulemavu; hii bima pamoja na kuwa vitambulisho sisi kwetu wamepata wengi sana, lakini bado dirisha lile lina dawa kiasi kidogo sana, wengi hawapatiwi, ukizungumza na wazee unaona wanalalamika kwamba dawa zile hawapatiwi zote na kuna baadhi ya vipimo hawapimwi na wazee kila wakati ni kuumwa, ni migongo, ni nini, lakini dawa hawapatiwi. Niombe kwa kweli Serikali iangalie wazee wetu wapatiwe dawa ambazo zinahitajika katika kile kitambulisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutakuwa hatuwatendei haki wadau ambao wamekuwa wakichangia huduma za afya katika mkoa wetu. Tumpongeze sana Mheshimiwa Asas m-NEC wetu wa Mkoa, kwanza kabisa ametujengea jengo la damu salama katika mkoa wetu, lakini ametujengea jengo la watoto njiti, vilevile ICU, jamani Mwenyezi Mungu ampe nini huyu baba, tunamshukuru sana. Pia kajenga jengo la wazee, zuri, Mheshimiwa Waziri aje atutembelee aone wazee wanaishi kwa raha mustarehe. Hii yote ni kazi ya m-NEC wetu wa mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama cha Mapinduzi Wilaya, pia kimeleta mashine za kufulia mashuka. Kwa hiyo hata Chama chetu cha Mapinduzi kinafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo kwa kweli na mimi nitoe pole kwa Mheshimiwa Mengi, pole nyingi sana kwa sababu ni baba ambaye ametufundisha mambo mengi sana na Mwenyezi Mungu amrehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Peter Msigwa ajiandae Mheshimiwa Janeth Masaburi

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Nianze na kumtanguliza Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza na kuwapongeza sana Wizara ya Uchukuzi na Ujenzi. Tumetembelea miradi yao tukiwa na Kamati ya miundombinu, miradi ni mizuri sana, wameitendea haki nchi yetu na wametekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye Mkoa wangu wa Iringa na niende kwenye changamoto kubwa za barabara za kiuchumi zilizopo katika Mkoa wetu wa Iringa. Tunazo barabara ambazo kwa kweli tunaomba Serikali ingezichukua na kuanza kuzifanyia kazi kwa sababu Mkoa wetu wa Iringa unakosa uchumi kwasababu ya barabara ambazo ni mbovu, hazipitiki mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo barabara kwanza inayokwenda katika Mbuga za Wanyama. Hii barabara imeshasemewa na Wabunge karibu wote wa Iringa. Hii barabara inakwenda kwenye Mbuga ya Wanyama ambayo ni ya pili kwa ukubwa kwa Afrika. Tulikuwa tunategemea kama hii barabara ingeisha kwa wakati, basi wananchi wa Iringa wangeweza kujiajiri kupitia hata hii barabara kwa utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, imekuwa inajengwa dakika mbili mbili…

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Grace Tendega.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda kumpa taarifa mzungumzaji anayezungumza kwamba barabara hiyo ya kwenda Ruaha National Park kilometa 104 ni barabara ambayo imeahidiwa na Hayati Rais wa Awamu ya Tatu, Rais wa Awamu ya Nne na Hayati Rais wa Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi kilometa zote kuanzia mwaka 2015 walikuwa katika upembuzi yakinifu na usanifu wa kina toka 2015. Kwa hiyo, ninapoona hivi, nataka kumpa taarifa kwamba hii hali ni mbaya na tumetengewa pesa ya kushika mfuko tu, shilingi milioni 1,500.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naipokea taarifa hiyo kwa sababu kwa kweli lazima Wabunge wote wa Iringa tuisemee kwa sababu inatusaidia wananchi wote wa Iringa. Naomba sasa Mheshimiwa Waziri aone umuhimu, kwa sababu tumeambiwa kwamba itakuwa kwenye package ya World Bank, lakini toka Mheshimiwa Marehemu yupo akiwa Waziri nilishawahi kuuliza swali na mpaka amekuwa Rais; naomba Mheshimwa Waziri hebu tupe kipaumbele kwenye hii barabara ambayo inakwenda kwenye Mbuga za Wanyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazo barabara nyingine ambazo ni za kiuchumi zinahitaji sasa kupewa kipaumbele. Kuna barabara ile ya Nyololo - Mafinga kilomita 40.4. Hii barabara hata Mbunge wa Mafinga kila siku anaizungumza. Kuna Mgololo, kuna Igoole - Kasanga kilomita 54 lakini kuna Kinyanambo C - Usokami ambayo inakwenda mpaka Kisusa; kuna Kinyanambo A – Sadani – Madibila, hizi barabara na zenyewe zipatiwe kipaumbele kwa sababu ni za kiuchumi ambazo tuna imani kabisa Serikali ikizichukua, basi Iringa itakuwa ni moto kweli kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunayo barabara nyingine ya Iringa - Idete hii barabara inaunganisha Jimbo la Iringa Mjini - Jimbo la Kilolo na kwa kweli hii barabara inakwenda Idete mpaka Mlangali mpaka inaenda kuunganisha Mlimba. Hii barabara itasaidia kutoboa, kwamba tutakuwa tunafika mpaka Morogoro na itakuwa mbadala kama kutakuwa kuna tatizo kwenye huu mlima wa Kitonga, hatutakuwa na haja ya kupita mlima wa Kitonga, tutatokea Morogoro kuja kufika mpaka Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna ile barabara ya Ilula, Mlafu, Mkalanga, Ipalamwa, Kising’a na Kilolo. Hizi barabara zote ni za kiuchumi. Tunaomba kwa kweli Serikali iziangalie ili uchumi uweze kufunguka. Kwa kweli hizi barabara mara nyingi hazipitiki hata Mbunge wa Kilolo juzi nilimsikia anaongelea. Kwa nini sasa kama alivyoshauri Mheshimiwa Kawawa, kuna maeneo korofi ambayo yanajulikana, ni kwa nini sasa yale maeneo korofi Serikali ingekuwa inaangalia kuliko kuanza kutengeneza kilomita labda mbili kutoka Iringa mjini, mbili kutoka Kilolo: ni kwanini sasa wasiangalie tu yale maeneo korofi halafu ndiyo waweke kipaumbele katika kutengeneza ili ziweze kupitika mwaka mzima? Kwa sababu zote zina maeneo korofi, siyo kwamba yote haipitiki, lakini tunachotaka ipitike mwaka mzima ili wananchi waweze kupitisha mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunayo barabara ile ya mchepuo ya Tumaini, kuchepusha yale magari mazito malori yasipite katikati ya barabara ambayo hata leo Mheshimiwa umesema kwamba ile barabara ya Tanzam malori yanapita mengi sana pale mjini kiasi kwamba kuna wakati itatokea ajali kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi Iringa pale hatuna sehemu ya kupaki magari, kwa hiyo, magari yakipaki pale barabarani yanaleta shida kwa sababu wafanyabiashara wanashindwa kufanya biashara zao, kwa sababu wakiweka tu magari TANROAD wanafunga yale magari na hapo hapo watu wanalipa karibu shilingi 150,000/= au shilingi 200,000/=, wafanyabiashara wanashindwa kufanya biashara. Sasa Serikali ione umuhimu hizi barabara zetu ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami ili zipitike mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu mfuko ambao wanawake huwa wanasaidiwa. Wizara ilikuwa inatoa fedha ili iwasaidie Wakandarasi wanawake kuwajengea uwezo ili tuwe na wakandarasi wengi wanawake. Nampongeza Mheshimiwa Eng. Ulenge ambaye nakumbuka wakati ule alikuwa kwenye hiki kitengo, sasa sijajua; changamoto kubwa ilikuwa ni ufinyu wa bajeti kwamba wanawake wengi hawajengewi uwezo. Sasa naomba hiki kitengo kitengwe fedha nyingi ili wanawake wengi waweze kuwa makandarasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo nampongeza binti mmoja katika barabara ile ya Tanzanite Bridge, tulikuta mtoto wa kike mdogo kabisa, yeye ndyo anasimamia ile barabara. Ni Engineer; kwa kweli alitu-impress sana sisi Wajumbe wa Kamati ya Miundombinu na tukasema kwamba ipo haja sasa kwa watoto wetu wengi wa kike wajengewe uwezo. Tunakupongeza Engineer Mfugale lakini tunaomba weka wanawake wengi pengine hata ukiondoka waachie hawa akina dada; na unajua akina mama sasa wanaweza na huu ni wakati wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niendelee kupongeza mradi wa SGR; kwa kweli tumepita katika eneo lote kuanzia hapa mpaka Dar es Salaam na tumekuta asilimia 50 ya wataalam ni vijana wetu. Kwa hiyo, hiki ni kitu kizuri ambapo wanawajengea uwezo na uwe utaratibu mzuri kwamba hata hawa wataalam wa makampuni haya makubwa yakiondoka, vijana wetu wanakuwa wamejengewa uwezo. Kwa hiyo, hili lilitufanya na sisi tukapongeza sana kwamba vijana wengi sasa ma-engineer tutapata kutoka hapa hapa Tanzania na wanajengewa mradi mzuri. Pia kuna fursa nyingi sana kwenye huu mradi ambazo tuliziona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze sana pia ujenzi wa uwanja wa ndege uliopo Iringa na tuliambiwa kwamba mwaka huu, huu tutaenda kuzindua ule uwanja wetu na tunaimani sasa tutafanya biashara kupitia huu uwanja, lakini kama haitajengwa ile barabara, bado tutakuwa tunahitaji kwa kweli mfanye kazi nzuri. Vile vile tunapongeza kwamba wananchi wameshalipwa kabisa, hawadai kitu chochote. Kwa hiyo, tunaomba Waziri azingatie hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nizungumzie kuhusu malipo ya Wakandarasi. Wakandarasi wengi bado wanadai. Tulipokuwa kwenye Kikao cha Road Board cha Mkoa wa Iringa, walikuwa wana changamoto nyingi sana kwamba hawalipwi malipo yao, wanadaiwa pesa nyingi kwenye benki, wanadaiwa TRA na walikuwa wanaomba kujengewa uwezo. Tumekuwa na miradi mingi na tulisema kwamba Wakandarasi wa ndani wajengewe uwezo na ikiwezekana pengine hawa Wakandarasi wa nje wakija, pengine zile kazi ndogo ndogo wapatiwe Wakandarasi wetu wa ndani ili pia iwasaidie, pengine wanaweza wakaachiwa vifaa na pia wakapewa uwezo mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo nakushukuru, naomba Mheshimiwa Waziri, zingatia Mkoa wetu wa Iringa, una changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nami nafasi ili kuchangia hoja iliyoko mezani. Kwanza kabisa nami naomba nitoe pongezi kubwa sana kwa Kamati zote ambazo zimewasilisha ripoti zao ili tuweze kuzijadili, kwa sababu wamewasilisha ripoti ambazo kwa kweli wamewasilisha vizuri sana nasi tumeweza kuzitambua na tunaweza kuzichangia vizuri. Moja kwa moja nami nianze na Mfuko wa Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Spika, tathmini ya ufanisi wa mfuko huo unaonyesha kwamba kuna vikundi 155 havikurejesha mikopo ya Bilioni 47 iliyotolewa katika vikundi mwaka 2019. Pia umebaini kwamba kuna mamlaka 83 za Serikali za Mitaa hazikuweza kuchangia jumla ya Shilingi Bilioni 6.26 katika vyanzo vyao vya mapato. Hili jambo siyo dogo, kumekuwa na hoja nyingi sana katika utoaji wa hii mikopo, Bunge letu lilitunga sheria ya utoaji wa ile asilimia 10, asilimia Nne kwa akina mama, asilimia Nne kwa vijana na asilimia Mbili kwa watu wenye ulemavu, sasa ni kwa nini sheria hii haitekelezeki? Kwa nini Halmashauri zinakuwa hazitekelezi hizi sheria, siku zote tumekuwa tukizungumzia hili jambo katika hili Bunge. Tumekuwa tukiuliza maswali tunaona yanajibiwa lakini bado tatizo linaendelea, zikija hoja bado tunaona hoja zile zinajirudia mara kwa mara. Kuna baadhi ya Halmashauri hoja zimejirudia miaka saba, kumi, au miaka mitatu ni kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Halmashauri zingine tunaona kwamba zinatoa fedha hewa katika vikundi, Halmashauri nyinginezo zinatoa fedha chini ya kiwango ya mikopo na Halmashauri nyinginezo zinabadilisha matumizi ya hizi fedha. Ipo haja Serikali sasa ipendekeze adhabu kwa Halmashauri ambazo hazitekelezi hii sheria ambayo tumeitunga wenyewe hapa Bungeni, kwa sababu imekuwa kila siku tunaongea lakini hakuna adhabu yoyote inayotolewa pengine ikitolewa leo adhabu hizi fedha zitaweza kutekelezeka na kila Halmashauri itatendewa haki, na wananchi wetu inapotolewa hii mikopo maana yake sisi tunapigania kwamba Serikali ilikuwa inayo nia njema kabisa kuhakikisha kwamba wanawake, vijana na watu wenye ulemavu waweze kukopeshwa ili ilete tija.

Mheshimiwa Spika, naomba nami niungane na watu wa Kamati kwamba sasa ipo haja kuwepo na akaunti maalum ya hizi fedha za kutoa na kukusanya. Itakukwa rahisi sasa kui-monitor ili iweze kuleta manufaa zaidi. Pia kuwepo na mpango mahsusi wa wanufaika kupatiwa elimu, kwa sababu bila elimu tumeona kwamba vikundi vingi sana vinapewa hii fedha lakini hawana elimu hata ya kuweza kufanya biashara ambazo wanapatiwa.

Mheshimiwa Spika, tumeona sasa hivi, tunavyo Vyuo vya VETA, tunavyo Vyuo vya Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri zetu na Mikoa yetu, ni kwanini sasa elimu isitolewe katika hivi vyuo vya VETA? Tumeona vijana wengi sana wanamaliza vyuo vya VETA bado hawana mkakati wowote hata wakisaidiwa kupewa hii mikopo ya vijana, mpaka vijana muda mwingine wanajishughulisha kwenye bodaboda hata wengine hawakupenda kukopa hizi bodaboda lakini kutokana na pesa ndogo sana ambayo vijana wanakopeshwa na akina mama. Unakuta kikundi kimoja kinapatiwa labda mkopo wa Shilingi Milioni Mbili akina mama 20 au vijana 10 wanapatiwa mkopo wa Milioni Tatu, matokeo yake wanaona bora tukinunua bodaboda tuizungushe ili iweze kutusaidia. Bado kungekuwa na mkakati, vijana wanaomaliza vyuo vya VETA, wamesoma wapatiwe mashine badala ya kupatiwa fedha, wanaweza wakapatiwa hata mashine ya kufyatua tofali, wakapatiwa mchanga, simenti na baadae Halmshauri iweze kuchukua ijengee labda shule na hospiatali. Utaona hawa vijana watakuwa na uhakika wa kulipa ule mkopo kuliko ilivyo sasa hivi vijana wanapatiwa fedha hawana elimu au utaalam wowote wa kuendesha hizi fedha na matokeo yake zinashindwa kurudishwa kwenye Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, unakuta kwamba sasa hivi vijana wamesomea mambo ya uvuvi, wamehitimu masomo ya mifugo na kilimo, hizi fedha bado baadhi ya Halmashauri tunapata fedha nyingi sana kwa ajili ya kilimo au uvuvi au mifugo. Kwa nini vijana wasipatiwe elimu ya ufugaji wa samaki, wakajengewa bwawa, wakanunuliwa samaki, wakapatiwa vyakula halafu baadae wakianza kurudisha tena kuna masoko mengi wakapatiwa hata hayo masoko, Kwa hiyo Halmashauri zinakuwa na uhakika kwamba hizi fedha ni lazima zitarudi kwa sababu ni revolving fund ambazo mtu akirudisha, vijana wengine wanakopa au akinamama wanakopa na watu wenye ulemavu pia.

Mheshimiwa Spika, kwa watu wenye ulemavu kuna miradi maalum ingetengenezwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu, kwa sababu tumepitisha kwamba mlemavu mmoja mmoja anaweza akakopa ama walemavu wawili. Sasa kungekuwa na miradi maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu wapatiwe vifaa na pia wasaidiwe kutafuta masoko ili iweze kuwasaidia kuliko ilivyo sasa hivi tunapoteza mapato makubwa bila sababu lakini kumbe nia ya Serikali ilikuwa nzuri sana kuhakikisha kwamba tunawasaidia watu wenye ulemavu, akinamama na vijana ili ulete tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulifanya ziara na tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri ambae ameteuliwa sasa hivi Mheshimiwa Angellah Kairuki, alipokuwa Katibu wa Wanawake kwenye Chama chetu hiki cha Wanawake hapa Bungeni, alitutafutia ziara nyingi sana kwenda kujifunza miradi ya akina mama. Kwa mfano, tulikwenda China, Uingereza na sehemu nyingi sana, tulikuta pale China akina mama wana miradi mikubwa sana kwa sababu wanavyo viwanda vidogovidogo vya ndani, sasa ifikie sehemu hata Halmashauri zetu, badala ya kuwapatia pesa tuwapatie viwanda vidogovidogo ambavyo kila nyumba ikiwa ina viwanda tayari hata ajira kwa vijana tutatengeneza ajira nyingi sana hata wenyewe tutajiajiri kwa kutumia viwanda vidogovidogo ambavyo viko katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tayari Halmashauri zetu zitapata chanzo cha mapato kwa sababu watalipa kodi za Halmashauri pia tutaongeza pato katika nchi yetu na ndivyo ambavyo hata Wachina wenzetu wanafanya vitu vingi ni kwa sababu badala ya kuwapatia fedha wanawapatia viwanda vidogovidogo ambavyo viko katika nyumba zetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ambacho nilikuwa nataka kuchangia ni kuhusu uteketezaji wa madawa ya binadamu kwenye vituo vya afya na katika hospitali zetu. Taarifa ya CAG ya mwaka 2020/2021 inaonesha kuwepo kwa wimbi kubwa kabisa la uteketezaji wa madawa. Kitu ambacho mimi nimejifunza hapa, utaona hivi vituo vya afya na Hosipitali za Wilaya, Mkoa zimekuwa zinalipia madawa kule MSD lakini unakuta kwamba haya madawa yanacheleweshwa kuletwa kwenye hospitali zetu kwa muda mrefu kiasi kwamba sasa muda mwingine yakiletwa inakuwa muda wa matumizi umekwisha. Kwa hiyo, matokeo yake sasa madawa yanateketezwa, kunatakiwa kuwepo na fedha tena ya kuteketeza hayo madawa. Vilevile tatizo kubwa wananchi wanakwenda kutibiwa, wanaandikiwa dawa na dawa hazipo. Huo ni uzembe, tunapoteza mapato makubwa wananchi wakitegemea kwamba watapata huduma za afya lakini matokeo yake hawapatiwi huduma za afya, dawa zinateketezwa na fedha za Serikali inaliwa, matokeo yake tunaletewa hoja kubwa kwa Serikali, hakuna kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilisahau kusema, tulivyokwenda China, tuliambiwa kwamba wao watu wanaoiba fedha ya Serikali adhabu yao ni kuuawa lakini sisi kwa sababu ya haki za binadamu hatuwezi kufanya kitu kama hicho, tufanye kitu kikubwa ambacho kitasababisha watu wawe na nidhamu ya matumizi ya fedha ambazo tunazipeleka kwenye Halmashauri zetu. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, mimi ninaomba uteketezaji wa hayo madawa….

SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati, hebu hapo kwenye mchango wa China na watu kuuawa na haki za binadamu hebu paweke vizuri.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nimesema hivi: tulipokwenda China kuangalia miradi ya akina mama, tulipokuwa tunapewa ripoti kwamba wao China, watu wakiiba fedha ya Serikali adhabu ni kifo, lakini kwa sababu Tanzania hatuna adhabu ya kifo kwa sababu ya haki za binadamu, basi angalau tutoe kitu kikubwa kitakachowafanya hawa watu wanaoiba mali za umma, wapewe adhabu kali ambayo itawafanya hata wananchi waone kwamba sisi wananchi tunachangia pato la nchi lakini watu ambao wanafanya uhujumu wa hii fedha kweli wanapatiwa adhabu ambayo inasababisha wananchi turidhike na kile wanachokifanya. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati, nilikusudia kusema hivi kwa sababu unazungumzia nchi, watu kuuawa, Bunge lisielekezwe upande huo, kwa hiyo huo mchango wa China na kuua watu, hata sisi tunayo adhabu ya kifo haijafutwa, tunayo adhabu ya kifo ila siyo kwa haya unayoyazungumzia. Kwa hiyo, hii habari ya China na mfano wa wao kuwa wanaua watu naamini na wao wanafuata utaratibu kama ambavyo na sisi tunayo adhabu ya kifo. Kwa hiyo, mchango wako hapo uondoe kwenye Hansard halafu weka hoja yako ni nzuri tu, inaenda vizuri sana bila huo mfano. Ahsante sana.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba basi Hansard iweze kutoa mambo ya kifo lakini kupoteza mali ya umma siyo nzuri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninataka kulizungumzia ni kuhusiana na michango ya NHIF. Kuna mapato mengi sana yanapotea. Yanapotea kwa sababu gani? Tumeona jana kuna Mheshimiwa Mbunge alizungumza kwa uchungu sana kwamba hata akinababa wanaambiwa kwamba wamejifungua iko kwenye madai yao kwamba wanaume wamejifungua na fedha ipo imekatwa NHIF. Tumeona sasa hivi wanao utaratibu mzuri sana, unatoa taarifa kwamba umetibiwa katika kituo fulani. Sasa kwa nini wasiseme kwamba wametibiwa kwa mfano, mimi labda nimetumia kadi yangu ya NHIF kwenye hospitali hata ya private, sasa niambiwe kwamba nimetumia kiasi gani? Kwa sababu tunaona kama kuna mapato mengine mtu anasingiziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mfano wa Mbunge mmoja alikwenda kutibiwa kwenye kituo cha afya, alipokwenda kutibiwa kwenye kituo cha afya, ana ulcers tu, akapewa dawa za ulcers, baadae akapigiwa simu kwamba ulikuwa umelazwa? Akasema sijalazwa lakini inaonesha kwamba amelazwa siku saba, katumia drip, wakati alikuwa ametumia dawa tu na mfano hai upo, Mbunge aliyepigiwa simu yupo. Kwa hiyo, NHIF basi ingekuwa wanafuatilia wanatuletea hizo taarifa za matibabu yetu pamoja na bills tumetibiwa kiasi gani itakuwa rahisi, hata kama sisi wenyewe Wabunge saa nyingine tunakwenda kutibiwa kwenye Mkoa mwingine basi taarifa ziletwe Bungeni kwamba Mbunge fulani katibiwa sehemu fulani na gharama zake ni kiasi hiki itakuwa rahisi hata kufanya reconciliation kwamba Bunge letu, Wabunge tumetumia kiasi hiki kuliko ilivyo sasa hivi, mtu unalimbikiziwa gharama ambazo zisizo zinakwenda kwenye Mfuko matokeo yake wanaua Mfuko bila sababu.

Mheshimiwa Spika, hivyo ninaomba Serikali yetu iangalie huu Mfuko kwa sababu ni muhimu na tunaenda sasa kupitisha Sheria ya Mfuko wa Bima ya Afya lakini kama kutakuwa hakuna control yoyote ya matibabu ya watu wanavyotibiwa itakuwa haina maana yoyote kwamba nia nzuri ya Serikali inakuwa inapotoshwa. Watu wachache wasifanye watu wakaichukia Serikali yao kwa sababu ya vitu vidogo sana.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa naomba nikushukuru sana na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anazozifanya. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri walio katika Wizara yake kwa kutuletea bajeti ili tuweze kuijadili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii imegusa kila eneo lakini yapo baadhi ya mambo ambayo nataka nipatiwe ufafanuzi:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu watu wenye ulemavu; niipongeze Serikali katika ukurasa wa 21 inasema inathamini mchango mkubwa wa watu wenye ulemavu katika maendeleo na kwamba wana haki sawa ya kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Hata hivyo, bado watu wengi wenye ulemavu wanapata mateso sababu Serikali haijaweza kutunga sheria kuhakikisha watu wanaomiliki vyombo vya usafiri wanahakikisha miundombinu inakuwa rafiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, walemavu wengi wamekuwa wakipata mateso makubwa sana hasa wale wenye baiskeli kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine wanapokuwa wanasafiri umbali mrefu. Bado majengo mengi sana hayajaweza kuwa na miundombinu rafiki ya kumfanya mtu mwenye ulemavu aweze kuyatumia kama vile shule, hospitali, vituo vya afya hata ofisi zetu za Serikali, mtu mwenye ulemavu anapotaka huduma katika majengo hayo imekuwa ni mateso kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua ni lini Serikali itaweka sheria kuhakikisha zinalinda haki ya mtu mwenye ulemavu. Pia bado wetu wenye ulemavu wengi na hasa wale wasio na uwezo wa kupata baiskeli wapo nyumbani hawapati hata haki ya kusoma. Nashauri Serikali ihakikishe kila mwenye ulemavu anapatiwa baiskeli bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilianzisha program ya kuwasaidia watu wenye ulemavu katika mkoa wangu, niliamua kuwathamini, kuwajali na kuwasaidia pale walipo, naelewa changamoto nyingi sana ambazo Serikali yetu inatakiwa kuzitatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu ya bure; niendelee kuipongeza Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kutoa elimu bila malipo nchini, imesisitiza kila mzazi kupeleka mtoto shule na asiyepeleka mtoto hatua kali itachukuliwa dhidi ya mzazi/mlezi huyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali imeweka mkakati gani kuhakikisha hawa watoto wa mitaani au watoto wanaojulikana kama ombaomba nao wanapata hiyo haki ya kusoma? Ni nani anayewajibika ili watoto hawa wasome? Swali hili huwa najiuliza kila siku lakini huwa nakosa jibu, ningependa kujua mkakati wa Serikali kuhusiana na hilo.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa ushauri au pendekezo langu kwa Serikali, kwa kuwa kuna shule za watu binafsi na shule nyingi zimekuwa zikitoza fedha nyingi lakini nazo zimekuwa zikitozwa kodi na Serikali, kwa nini Serikali isiweke utaratibu wa kuwapeleka hawa watoto katika shule hizo ili zile shule zinazokubali kuwachukua na kuwasomesha hawa watoto wa mtaani shule hizo zipunguziwe kodi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu madeni ya wazabuni, wazabuni wa nchi hii bado wana mateso makubwa sana pamoja na kuwa walijitahidi kutoa huduma kwa Serikali yetu, kuna baadhi ya wazabuni ambao toka awamu zilizopita wamekuwa wakifuatilia malipo yao bila mafanikio. Serikali itambue kwamba wazabuni hawa wengi wao ni wale waliochukua mikopo benki na kuna wazabuni ambao wamesababishiwa kutaka kuuziwa dhamana zao walizoweka rehani ili wapatiwe mikopo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itambue kuwa wazabuni hawa pia wanadaiwa na kodi ya mapato, kwa sababu sheria inasema ukishatoa invoice kwa mzabuni wako unatakiwa ulipe kodi, sasa wanalipa kutoka wapi wakati bado hawajalipwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kuhakiki madeni ya wazabuni bado hatma ya malipo haijajulikana. Ningependa kujua Serikali hii ya Awamu ya Tano imejipanga vipi kuhakikisha wazabuni wanalipwa kwa wakati ili kumwondolea adha ambayo mzabuni amekuwa akiipata na imesababisha wazabuni wengi kufilisika na kufunga biashara zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali wa kutoa milioni hamsini kila kijiji; naendelea kutoa pongezi zangu kwa Serikali na Rais wa Awamu hii ya Tano kwa kuwa na mpango wa kupeleka milioni 50 kila kijiji. Sasa napenda kujua, Serikali imejipangaje kutoa elimu ya kuwatayarisha walengwa ili kuhakikisha pesa hizi zitakapoanza kutolewa zinawafikia walengwa na zinawasaidia, pia kuweza kurudishwa ili ziweze kuwa na mzunguko, kwa kuwa ukimpatia mlengwa akazirudisha zitasaidia walengwa wengi kufikiwa. Tuna rundo kubwa sana la akinamama ambao wameweza kuwa na uthubutu wa kufanya biashara, lakini hawana mitaji, sasa hili jambo litakuwa ndiyo suluhisho ya mambo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira zisizo rasmi; napenda kujua ni lini Serikali itarasimisha ajira zisizo rasmi? Kwa mfano, Mkoa wetu wa Iringa ni Mkoa ambao vijana wengi wamekuwa wakipata ajira ya kufanya kazi za ndani (house girl au house boy), pia tumekuwa na mkataba wa Kimataifa na nchi yetu kuridhia, bado ajira hii haijarasimishwa imekuwa ikisababisha vijana wengi kufanyiwa vitendo vya kikatili, kunyanyaswa, kubakwa, kupata mimba zisizotarajiwa na kuambukizwa UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua ni lini ajira hii itarasimishwa ili vijana wetu waweze kutendewa haki na hata kujiunga katika Mifuko ya Jamii, kuwekewa bima ya afya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mauaji ya vikongwe; haya mauaji ya vikongwe hasa Mikoa ya Kanda ya Ziwa yamekuwa ni tishio na mauaji haya yamedumu kwa muda mrefu sana. Ningependa kujua Serikali imejipanga vipi kukomesha ukatili huu wanaofanyiwa vikongwe kwa kushirikishwa na imani za kishirikiana? Je, toka mauaji haya yameanza kufanyika ni vikongwe wangapi wameuawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kumaliza miradi ya zamani. Ningependa kujua mpango wa Serikali kuhakikisha inamaliza miradi iliyochukua muda mrefu kukamilika. Kwa mfano, katika Halmashauri yetu upo mradi wa machinjio, mradi huu umechukua muda mrefu sana kukamilika. Ni imani yangu kuwa mradi huu ukikamilika Manispaa yetu itakuwa na chanzo kizuri sana cha mapato na pia Halmashauri itaongeza ajira kwa vijana wetu, hivyo ningeshauri Serikali ifanye tathmini ya vile vyanzo ambavyo vinaweza kutuongezea mapato na miradi yake ipewe kipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji; niendelee kuipongeza Serikali kwa kuendelea kutekeleza Program ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa lengo la kuwapatia wananchi huduma ya maji safi, salama na ya kutosha. Imani yangu ni kuwa, kama program hiyo itakamilika, nia ya Serikali kumtua mwanamke ndoo ya maji kichwani itatimia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa hauna tatizo la maji, bali tatizo kubwa ni usambazaji wa maji. Kwa mfano, Wilaya ya Kilolo ina mito mingi, Serikali inashindwaje kutoa maji kutoka kwenye Mto Lukosi, Ruaha na Mtitu? Nina imani kabisa kama Serikali ingesambaza maji kupitia vyanzo vya mito hii, ingeweza kutumia gharama nafuu sana ya uhakika kuliko kuchimba visima visivyokuwa na tafiti za kutosha na kusababisha pesa nyingi kutumika katika tafiti badala ya kutumia vyanzo vya mito, kwa sababu maji yanapokosekana ni mwanamke ndiye anayeteseka. Tunaomba ile ahadi ya kumtua mama ndoo kichwani ikamilike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma muhimu katika Wilaya mpya; kuna Wilaya ambazo zimeanzishwa muda mrefu sana, lakini bado hazijapatiwa huduma muhimu. Kwa mfano, Wilaya ya Kilolo ilipata hadhi ya kuwa Wilaya toka mwaka 2002, mpaka leo hii Serikali haijaweza kujenga Hospitali ya Wilaya, Makao Makuu ya Polisi, Mahakama ya Wilaya, pia barabara inayounganisha Makao Makuu na Wilaya mpaka leo hakuna lami pamoja na Halmashauri kuweka jitihada ya kutenga maeneo kwa ajili ya huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina wasiwasi hata hizi ahadi za Serikali za kujenga Wilaya mpya kama zitatekelezeka, ningependa kujua mpango wa Serikali wa kuhakikisha hizi Wilaya zilizoanzishwa muda mrefu utekelezaji wake upo vipi, ukamilishaji wa hizo huduma katika Makao Makuu ya Wilaya, kwa sababu wananchi wamekuwa wakipata shida sana kuzifuata hizo huduma na hasa kutokana na changamoto za miundombinu ya barabara zetu za vijiji zilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia bajeti iliyoletwa Mezani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kurudi tena kwa mara ya pili katika Bunge hili maana bila yeye nisingekuwemo.
Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia bajeti hii, naomba kwanza nishukuru na nikipongeze sana Chama changu cha Mapinduzi kwa ushindi wa kishindo na niwapongeze Wabunge wote wa Chama cha Mapinduzi. Vilevile niendelee kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifanya. Nimpongeze pia Waziri Mkuu na Mawaziri wote wamekuwa wakifanya kazi nzuri na kwa umakini mkubwa sana. Nimpongeze Spika, nikupongeze na wewe Naibu Spika, nipongeze pia na Wenyeviti wote wa Bunge kwa kazi nzuri mnayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze pia Rais wa Zanzibar kwa ushindi wa kishindo kikubwa alichokipata kwenye uchaguzi wao na sasa hivi Baraza la Uwakishilishi ni wana-CCM watupu. Najua sasa watafanya kazi nzuri sana kwa sababu tulipokwenda China labda niwakumbushe wenzangu walioenda China wenzetu wa China walisema kwamba Tanzania mnachelewa kwa sababu ya upinzani. Wenzetu kule chama ndiyo kinachoongoza Serikali, kwa hiyo tulivyokwenda hata na wapinzani walisema kwamba hawa kazi yao ni kuwinda yale mabaya. Kwa hiyo, naamini kwamba Zanzibar watafanya kazi nzuri sana, waendelee kufanya kazi wawakilishe vizuri chama chetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kushukuru tu, naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa ujenzi wa daraja la Igumbilo ambalo lipo katika Jimbo la Iringa Mjini. Lile daraja kwetu lilikuwa ni tatizo kubwa. Kila mwaka watu walikuwa wanakufa kwenye lile daraja kwa sababu kuna shule ya sekondari, kuna chuo sasa ujenzi wa lile daraja najua kwamba maafa ya vifo vya kila siku pale Iringa tumekombolewa. Kwa hiyo naamini kwamba uchaguzi ujao, najua Mama Mbega alitolewa kwa ajili ya lile daraja, tumeshajenga Jimbo litarudi tu kwenye Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kuchangia kuhusu ucheleweshaji wa fedha za miradi katika Halmashauri zetu. Kumekuwa na ucheleweshwaji mkubwa sana wa fedha za miradi katika Halmashauri na kusababisha miradi hii kuongezeka gharama kwa kiasi kikubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Manispaa yetu ya Iringa Mjini uko mradi ule wa machinjio ya kisasa wa Ngelewala. Ule mradi kwa kweli ulipoanza gharama yake ilikuwa ndogo lakini sasa hivi kadri unavyocheleweshwa ule mradi unaendelea kuongezeka gharama. Kwa sababu mpaka mwaka jana bajeti iliyopita tulitakiwa tutumie shilingi milioni 700 ili kumaliza mradi ule, lakini sasa hivi zinahitajika shilingi 1,400,000,000 ili mradi ule uishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, ule mradi utatunufaisha sana sisi Wanairinga kwa sababu kwanza tunategemea kupata ajira kama ya vijana 200 mradi utakapokamilika. Vilevile tunajua kwamba mradi ule utakapokamilika Halmashauri yetu itaongeza mapato. Pia kwa sababu yale ni machinjio ya kisasa tunategemea kwamba nyama itakayochinjwa pale itasafirishwa nje tutaongeza pia pato la fedha za kigeni. Kwa hiyo, labda Serikali ingefanya upembuzi yakinifu kuangalia ile miradi ambayo itasaidia kuongezea mapato kwenye nchi hii au kwenye Halmashauri zetu, hii ingemalizika kwa haraka zaidi ili iweze kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kuchangia kuhusiana na Serikali kutokamilisha miundombinu katika wilaya zetu. Katika Mkoa wetu wa Iringa, Wilaya ya Kilolo, nilishawahi kuuliza swali la nyongeza kwamba ilipata hadhi mwaka 2002 lakini mpaka leo miundombinu yake mingi sana bado haijakamilishwa katika makau makuu. Kwanza, Jimbo lile lina changamoto kwamba kuna wananchi wanaoishi mabondeni na kuna wanaoishi milimani. Kwa hiyo, utakuta kwamba kutokuwepo miundombinu kwenye makao makuu wananchi wanapata shida sana. Hakuna Hospitali ya Wilaya ya Serikali, hakuna Mahakama, Mahakama ya Wilaya wanaendeshea kwenye Mahakama ya Mwanzo. Vilevile Makao Makuu ya Polisi hayapo katika Makao Makuu ya Wilaya. Kwa hiyo, Serikali ingeangalia kwa sababu nia ya Serikali kuanzisha Wilaya ni kusogeza huduma kwa wananchi. Sasa kama hamuweki huduma kwa wananchi hata ile nia ya kuanzisha hizo Wilaya inakuwa bado haisaidii kitu chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niwazungumzie wazabuni. Madeni ya wazabuni kwa kweli yamekuwa mwiba sana. Wazabuni wengi wanadai sana na wengi wao kwanza wamekopa benki na wengi wao wanadaiwa mpaka kodi za mapato. Kwa hiyo, sasa nia ya kuwasaidia hawa wananchi wenye kipato cha chini inakuwa hamna kwa sababu kama wamekopa wakauziwa zile dhamana zao kwa ajili ya madeni ambayo wanadai Serikali naona itakuwa hatuwasaidii. Kwa hiyo, naomba suala hili lipewe kipaumbele ili wazabuni kwenye halmashauri zetu zote au kwenye Serikali yetu yote waweze kulipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine labda nielezee kuhusu barabara zetu za Halmashauri. Kumekuwa na tofauti kubwa sana kati ya barabara za Halmashauri na za TANROADS. Huwa najiuliza ni kwa nini kwa sababu hata kule kuna wataalam, labda kama mnapeleka pesa kidogo mngepeleka pesa nyingi ili na zenyewe ziwe na uimara kwa sababu barabara za Halmashauri zinajengwa temporary sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa…….
NAIBU SPIKA: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.
MHE. RITTA E. KABATI: Naomba niunge mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani kwetu. Naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza na pongezi kwa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye kwa kweli amefanya kazi nzuri sana katika kuhakikisha kwamba mwanamke anatuliwa ndoo kichwani. Zamani tulifikiri siasa lakini tunaona kabisa ana nia na anadhamira ya kweli kuhakikisha kwamba wanawake sasa tunatuliwa ndoo kichwani, na amejua kutuheshimisha sisi wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niungane na Waheshimiwa Wabunge wote kumpongeza Waziri wetu, Mheshimiwa Jumaa Aweso, amefanya kazi nzuri sana Pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Prisca Mahundi. Ana misemo yake usione vinaelea vimeundwa. Mheshimiwa Aweso anafanya kazi nzuri kwa sababu kuna mchango wa akina mama wale wawili ambao leo alitutambulisha pale juu, tena akina mama shupavu; wamemfanya atulie na kuzingatia kazi na Wizara inaenda vizuri. Tunawapongeza sana, utupelekee salamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona kobe yuko juu ya mti ujue amepandishwa. Niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kumpandisha Engineer Kemikimba kuwa Katibu Mkuu, lakini vilevile kumpa unaibu Katibu Mkuu Cyprian Luhemeja. Tuseme sasa upele umepata wakunaji na Wizara itaendelea vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sijawatendea haki kama sitampongeza Mkurugenzi Mkuu wa IRUWASA Eng. Kidegalu, lakini pia Meneja wetu wa Iringa Eng. Joyce, wanafanya kazi nzuri sana ya kuhakikisha kwamba vijiji vyetu vya Iringa vinapata maji na wanatekeleza miradi yao vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Mkurugenzi wa IRUWASA Engineer Kalanje wameubeba Mkoa wetu wa Iringa.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa tu mzungumzaji, na nimuongezee tu taarifa yake kwamba ni sehemu ya Mawaziri wa ukituma message wanajibu, ukipiga simu wanapokea. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hata usiku wa manane tukimtumia message anapokea. Mkoa wa Iringa umekuwa wa kwanza katika utoaji huduma za maji safi na mazingira kati ya mikoa 26, ndiyo maana nimewapongeza sana viongozi wetu wa Mkoa wa Iringa. Tunashukuru Wizara kwa kuipatia IRUWASA miradi mikubwa ya kuboresha huduma za maji katika Manispaa ya Iringa, katika Miji ya Kilolo na Ilula kupitia chanzo cha Mto Mtitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wametoa kibali cha kutekeleza miradi ya kuongeza chanzo cha maji kata ambazo zilikuwa hazijapatiwa maji, nawapongeza sana Wizara ya Maji. Kwa mfano mji wa Ilula tumeweza kupata milioni 445.7, Mji wa Kilolo milioni 413.8. Tunaomba sasa tupatiwe sasa hiyo advance payment ya milioni 413.3 ili sasa mabomba yanunuliwe ili kazi ya usambazaji iweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na suala la upotevu wa maji. Nimeona Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamezungumzia upotevu wa rasilimali ya maji. Pamoja na rasilimali za maji kuwa adimu lakini kuna upotevu kati ya asilimia 30 na 40. Hii itaweza kudhibitiwa endapo kutafanyika matengenezo, kwa sababu kumekuwa na matengenezo ya mara kwa mara. Mabomba mengi yamekuwa chakavu sana na miradi mingi imekuwa ya muda mrefu, haikarabatiwi. Sasa, kama itakarabatiwa basi angalau tutapunguza upotevu wa maji mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini changamoto nyingine ni pamoja na upungufu wa watumishi, hasa fani ya ufundi sanifu na wahandisi. Lakini tunacho Chuo cha Maji, tena sasa hivi vijana wengi sana wanakwenda kusoma pale. Tunaomba sasa Serikali iwatumie wale vijana ili wapunguze upungufu ambao uko katika mikoa yetu ikiwepo hata na Mkoa wa Iringa. Pia kuna wafanyakazi wengi sana wana vibali tu, hawaajiriwi. Siku nyingi sana tumekuwa tukisema, kwamba saa ifike sehemu Serikali itoe vibali, kwa sababu hizi mamlaka zina uwezo wa kuwalipa mishahara, ili vijana hawa wasiendelee tu kuwa kwenye zile mamlaka miaka miwili mikataba miaka mitatu; na hasa Dar es Saalam ulikotoka Naibu Katibu Mkuu, na wewe unajua. Sasa waajirini wale vijana basi sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pia kuna tatizo la changamoto ya vitendea kazi zikiwepo gari, hasa Mkoa wetu wa Iringa pia kuna tatizo kabisa la ukosefu wa magari katika wilaya zetu zote. Tunaomba sasa Mheshimiwa Aweso awe na mkakati wa kuhakikisha kwamba vitendea kazi vinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Wizara kwa kuanza mradi wa maji katika miji 28, hongera sana. Mradi huu ni wa siku nyingi, tumeuliza maswali mpaka tumechoka; lakini sasa hivi tunaona sasa umeanza kutekelezeka. Tumeona mkandarasi ameanza kazi hata pale katika Mji wa Mafinga tumepata tank la lita 2,000,000 pale Changarawe, kwa hiyo tunaapongeza sana. Vilevile kuna mradi wa Matanana na Itimbo, visima vimeshachimbwa bado fedha ya usambazaji. Sasa, tunaomba basi Wizara ituletee ili wanawake waendelee kufaidika na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye Jimbo letu la Isimani kwa Mheshimiwa Lukuvi tunaeona kuna mradi ule wa Kilolo – Isimani, tayari asilimia 90 umetekelezeka, na ule mradi unaanzia katika Kata ya Lugalo tunaomba pale kata zote au vijiji vyote vipatiwe maji sasa fedha ya usambazaji ndiyo inahitajika pia. Kuna mradi wa Pawaga unahitaji treatment plant, wananchi wanakunywa maji machafu sana. Hiyo yote ni fedha tunaihitaji Mkoa wa Iringa. Tuna miradi mingine tena bado kama mradi wa Kilolo. Mradi wa Kimara tunashukuru kwamba angalau umeshakamilika na wenyewe bado usambazaji. Mradi wa Uwambingeto unaendelea, na sasa uko asilimia 51, mradi wa Ifuwa tulipata bilioni 2.2 mkandarasi kalipwa asilimia 20 tu na maradi umesimama. Tunaomba pesa ende pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Kihesa – Mgagao – Masege wananchi wanapata shida mno, lakini bado uko kwenye uzabuni kila siku wanarudia tunaomba kazi ifanyike. Mradi wa Kata ya Kalenga kwa Mwenyekiti wetu. Kuna mradi wa Tanangozi – Tosamaganga mpaka Lupalama unahitaji ukarabati tu, tunaomba fedha ipatikane. Kata ya Nzii ma – tank mawili tayari tunaomba kazi ya usambazi maji. Lakini pia tunayo kata Mufindi Kusini, Ihoanza Malangali, Igunda. Mradi wa vijiji tisa, mradi wa Mtambula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee sasa kuhusu upungufu wa rasilimali maji. Takwimu zinaonesha upatikanaji wa maji kwa Mtanzania tangu tumepata uhuru hadi sasa. Wakati wa upatikanaji wa uhuru maji yalikuwa wastani wa lita za ujazo 10,000 kwa mtu mmoja kwa mwaka, lakini wastani huo umepungua sasa hivi ni lita za ujazo huo huo 2,250, ambao ni sawa sawa na upungufu wa lita 7,750 sawa sawa na asilimia 77.5. Upungufu huo umechangiwa na sababu zifuatazo; ongezeko la watu na mifugo, uharibifu wa mazingira, uchafuzi wa vyanzo vya maji, shughuli za binadamu, kilimo, ufugaji na mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwaka 2022 Serikali ilifanya mabadiliko ya sheria, lakini sasa tunaomba Serikali ione umuhimu wa kuzingatia zile sheria ili wananchi tuweze kupatiwa. Haya maji bila kufanya hizi sheria zikawa zinafanyika kazi; maana tunaona sheria zinatungwa lakini utekelezaji wake unakuwa sio mzuri sana. Kwa hiyo tunajitahidi vyanzo vingi vinakuwa vinaharibiwa. Tunaomba sasa Serikali isimamie kikamilifu ili tuweze kulinda vyanzo vya maji na mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nampongeza Mkurugenzi wa Dodoma wa Maji (DUWASA) amejitahidi sana, kuna population kubwa sana hapa Dodoma. Lakini juzi tulienda pale Mtera tulienda na Waziri wa Maji, Waziri wa Fedha, Waziri wa Mazingira na Waziri wa Nishati. Tumeona kabisa mambo ni mazuri pale tunaweza tukachukua maji kuyaleta Dodoma, kuliko kwenda kuchukua maji kule Mwanza kuyaleta hapa Dodoma gharama itakuwa kubwa sana. Mimi naona tuangalie huu mradi, kwanza hapa Jirani, kutoka Mtera kuja hapa. Sisi zamani tulikuwa tunafikiri labda itakuwa tatizo kubwa sana kuchukua yale maji ya Mtera, lakini jinsi tulivyoelezewa, alivyoelezea Waziri wa Nishati, wa Mazingira na wa Maji tumeona kumbe inawezekana. Kuna maji mengi sana yanafunguliwa yanapotea pale. Sasa basi yaletwe hapa Dodoma ili yaweze kusaidia wananchi, ili wananchi wa Dodoma waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba sasa Serikali iangalie hizi mita za maji, tuwekewe mita za maji kama ilivyo TANESCO, kwa sababu wananchi wengi wanalalamikia kwamba prepaid meter…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa…

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja mkono asilimia 200.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze na kumpongeza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji na watendaji wake kwa kuwasilisha hotuba ya bajeti yao hapa Bungeni ili tuweze kuijadili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ambayo nilikuwa napenda kupatiwa ufafanuzi na kutoa ushauri kwa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, viwanda vilivyobinafsishwa. Serikali iliamua kubinafsihsa viwanda vilivyokuwa vya Serikali na kubinafsishwa kwa wawekezaji lakini bado tunaona licha ya kuwa viwanda hivyo havifanyi kazi lakini vingine vimebadilishwa hata matumizi na vingine vimegeuzwa kuwa maghala ya kuhifadhia bidhaa au mazao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mpango mkakati gani kwa sababu awamu hii Serikali ina mpango wa kufufua viwanda na ningependa kujua hatua gani watachukuliwa wawekezaji hao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ningependa kujua katika ujenzi wa viwanda je, itazingatia katika maeneo yenye malighafi ili kupunguza gharama za kusafirisha malighafi kutoka zinakopatikana mpaka viwandani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Iringa hasa katika Jimbo la Kilolo asilimia kubwa kuna kilimo cha nyanya, pilipili na vitunguu, lakini wakulima wamekuwa wakipata shida sana kupata masoko kwa kuwa Serikali inahimiza ujenzi wa viwanda na kuna eneo la EPZ je, mkakati wowote umewekwa na Serikali ili kupata mwekezaji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, maeneo yaliyoteuliwa na EPZ. Kwa kuwa Serikali ilitenga maeneo mengi sana kwa ajili ya uwekezaji katika viwanda lakini maeneo mengi bado wananchi hawajalipwa fidia likiwemo lililotengwa katika Mkoa wetu wa Iringa. Nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanalipwa ili maeneo hayo yaweze kutumika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubovu wa barabara zinazokwenda katika viwanda. Nini mpango wa Serikali kuhakikisha barabara zote zinazokwenda katika viwanda zinajengwa kwa kiwango cha lami na barabara hizo zinahamishwa kutoka kuwa za Halmashauri na zinakuwa za TANROAD.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha bajeti hapa Bungeni ili tuweze kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ambayo nilikuwa naleta ili kupatiwa ufafanuzi na kutoa ushauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viwanja vilivyojengwa kwa ajili ya michezo, naomba Serikali inipatie majibu kuhusu viwanja vilivyotengwa kwa ajili ya michezo na Halmashauri zetu nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanja hivi watendaji wa Halmashauri waliamua kuvigawa na vikafanyiwa uvamizi yakajengwa majengo na baadaye Serikali ikatoa tamko kuwa wavamizi na maeneo ya wazi yaliyotunzwa kwa ajili ya michezo wabomoe lakini tamko hilo halijatekelezeka mpaka leo. Na kila siku tumekuwa tukiuliza maswali kuhusiana na jambo hilo lakini yanajibiwa kisiasa zaidi. Sasa naomba kujua jambo hili, Serikali imelichukulia vipi kwa sababu hatuwatendei haki vijana wetu, vipaji tunavitengenezea vipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kujua sheria za vyombo vya habari ni lini italetwa hapa Bungeni, kwa sababu tunaamini kuwa sheria hii ndiyo muarobaini wa matatizo yote katika vyombo vya habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu michezo ya UMISETA na UMISHUMTA. Michezo hii kwa sasa haina ari kabisa, ni imani yangu kama Serikali ingeamua kuwekeza mikono katika shule za msingi na sekondari zingeweza kuibua vipaji na tungeimarisha michezo yetu hapa nchini na kupata wachezaji bora. Inasikitisha kuona kuwa michezo ya shule za sekondari na msingi inapoanza shule nyingi watembeze mabakuli ya kuomba omba vifaa vya michezo mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Tanzania tutakuwa na Vazi letu la Taifa?. Serikali imekuwa kila mara ikitupatia taarifa kuwa Vazi la Taifa lipo katika mchakato. Ifike wakati tuambiwe kama imeshindikana tuambiwe ili tusiendelee kusubiri jambo lisilo na mwisho. Ni fahari kubwa kutambulika kwa mavazi kama zilivyo nchi nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini Serikali bado haiwezi kutoa kipaumbele timu ya wanawake, mbona timu ya Taifa inatafutiwa mpaka kocha wa kigeni kwa nini timu ya Twiga bado mpaka leo wanatembeza bakuli tu wanapokuwa na mashindano? Ni lini watapewa fungu au kutengewa katika Bajeti ya Serikali? Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha bajeti yao hapa Bungeni. Yapo mambo ambayo nilikuwa napenda kupata ufafanuzi wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanja vya ndege; ukisoma kitabu cha hotuba ya Waziri, ukurasa wa 90 – 91 unaeleza kuwa kupitia TCAA Serikali itaendelea kusimamia uboreshaji wa viwanja vya ndege na kiwanja cha ndege cha Nduli kikiwa kimojawapo. Lakini ukiangalia hali halisi ya kiwanja cha ndege cha Nduli kipo katika hali mbaya sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanja kina matatizo makubwa sana katika njia ya kurukia na kutua ndege (runways), kiwanja hakina fence, kila siku mifugo inapita katikati ya kiwanja. Kutokana na mafuriko yalijitokeza mwaka huu kiwanja kimeharibiwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2015 safari za ndege zilikuwa 2,300. Idadi ya abiria kwa mwaka 2015 walikuwa 8,300 hivyo ni ongezeko la asilimia 198 kwa safari za ndege katika kipindi cha miaka mitano. Kuna ongezeko la wasafiri wanaosafiri kwa ndege, ni asilimia 90 kwa kipindi cha miaka mitano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mbuga ya wanyama ya Ruaha; kama kiwanja hiki kitakamilika kwanza tutaongeza utalii na pia tutakuza uchumi wa Mkoa na Taifa zima. Naomba kujua kama kiwanja hiki kitajengwa kwa sababu katika mpango kipo, lakini muda ndiyo leo Waziri atupe jibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara za kiuchumi mkoa wa Iringa. Serikali ya Awamu hii ya Tano, sera yake ni ujenzi wa viwanda ili kukuza kwa uchumi wa nchi na kutengeneza ajira kwa wananchi. Katika mkoa wetu wa Iringa barabara nyingi za kiuchumi bado hazijaweza kujengwa kwa kiwango cha lami pamoja na kwamba katika hotuba yake kuna baadhi zimetengewa fungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kilolo; barabara ya Ipogolo - Kilolo, makao makuu, hii barabara inaunganisha Mkoa na Wilaya kilometa 37, lakini iliyojengwa kwa lami ni kilometa saba tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mufindi; kuna kiwanda cha karatasi, viwanda vya chai, msitu mkubwa; barabara zake ni Mafinga - Mgololo - Changalawe kupitia vijiji vya Sao Hill, Mtila - Matana kutokea Nyororo, Nyororo – Kibao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu reli ya kati; ili kuponya barabara zetu ni vema Serikali ikaijenga. Ushauri wangu ni kuwe na TANRAIL ambayo itafanya kazi kama TANROADS kuweza kusimamia masuala ya reli nchini, mfano reli ya kati, reli ya TAZARA, reli mpya kwenda DRC, hii ya Tanga - Uganda, Tanga - Kigali; itasaidia kubeba mizigo mingi, itasaidia kulinda barabara zetu, itasaidia kupunguza gharama, itasaidia kufungua fursa ya ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli ya TAZARA; muda mrefu Serikali inazungumzia kupitia upya mkataba wa Sheria za TAZARA, je, Serikali imefikia wapi? Ni kwa nini kwa upande wetu tusitumie reli ya TAZARA kwa usafirishaji wa ndani ya nchi, tuliambiwa upande wa Zambia wanafanya hivyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi mishahara ya wafanyakazi wa TAZARA imefikia wapi, hakuna tena mgogoro? Naomba kupata majibu ya Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi hii adimu. Kwa sababu nilishaongea naomba nianze moja kwa moja kwenye mada, naunga mkono hoja ya hotuba hii ya miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze moja kwa moja na ujenzi wa viwanja vya ndege na moja kwa moja nielekee katika Mkoa wangu wa Iringa. Kiwanja cha Nduli ni kiwanja ambacho toka nimeingia hapa Bungeni miaka mitano iliyopita, siku zote nimekuwa nikichangia hotuba ya Uchukuzi lakini kiwanja hiki tumeambiwa kwamba kipo katika mpango wa ujenzi wa vile viwanja 11. Haya majibu tulishapata toka hotuba ya Bunge lililopita, sasa ni lini hasa Kiwanja cha Nduli kitajengwa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hakijajengwa hiki kiwanja kina changamoto nyingi sana na najua kwamba ujenzi wa hiki kiwanja utasaidia sana kukuza uchumi wa Mkoa wetu wa Iringa, hata Taifa zima. Kwa sababu tunategemea sana ile hifadhi ya Ruaha ambayo tunajua kwamba watalii wengi sana tungewapata na tungeweza kupata ajira kwa vijana wetu na vilevile tungeweza kabisa kuongeza kipato cha utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja huu una changamoto nyingi sana. katika njia zile za kuruka na kutua (running way) kuna makorongo, yaani sio ma-corrugation, zile njia ni balaa, kwa sababu mwaka 2012, mwaka 2015 kulishawahi kutokea ajali ya ndege ya Auric. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri au na ile Kamati ingepita kuona, wakati wowote tunaweza tukapata matatizo. Ule uwanja sasa hivi hauna uzio, mara nyingi sana mifugo inakatiza katikati ya uwanja na vilevile bei ya ndege ni kubwa sana kwa sababu hakuna kituo cha mafuta. Kwa hiyo, inasababisha nauli inakuwa kubwa sana. Ningeomba kabisa uwanja huu ukakaguliwe mapema na ikiwezekana katika vile viwanja 11 basi kiwe cha kwanza kujengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia na ujenzi wa barabara za kiuchumi katika Mkoa wetu wa Iringa. Kwa kuwa Serikali hii ya Awamu ya Tano imeweka kipaumbele kabisa kujenga viwanda kwa ajili ya kujenga uchumi na kufufua viwanda vyetu nchini ili kuongeza ajira na pia kuongeza uchumi katika nchi yetu. Katika Mkoa wetu wa Iringa zipo barabara za kiuchumi ambazo siku zote Wabunge wangu wa Mkoa wa Iringa wamekuwa wakizizungumzia kwamba zijengwe kwa kiwango cha lami ili ziweze kupitika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kwenye Mkoa wetu wa Iringa, kwanza kabisa kuna Kiwanda kile cha Mgololo cha Karatasi, kuna Viwanda vya Chai ambavyo viko pale Mufindi na kule Kilolo. Vile vile kuna msitu na kuna hifadhi, lakini barabara zake zote za kiuchumi hazina lami, sasa utakuta malori yanapokwenda kuchukua bidhaa na kuna malighafi nyingi tu ambazo zingesaidia kwenye viwanda lakini wanapokwenda kuchukua zile malighafi wakati wa mvua malori yanakwama mno. Kwa hiyo, naomba kabisa Serikali sasa iangalie na izipe uzito. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kwenye kile kitabu, kuna baadhi ya barabara zimetengewa japokuwa ni finyu sana, lakini naomba sasa ungefanyika upembuzi yakinifu, ile miradi ya kiuchumi, barabara zile za kiuchumi zianze kujengwa ili kusaidia uchumi kwenye nchi hii. Labda hata nizitaje kidogo, kuna barabara hasa inayokaa katika hifadhi, Ruaha National Park, hii nafikiri ipewe kipaumbele kikubwa sana katika mkoa wetu, kwa sababu ile hifadhi ni ya pili katika Afrika. Halafu katika Wilaya ya Mafinga kuna ile barabara ya Mafinga-Mgololo, kwenda Shangalawe kupitia Sao Hill, Mtula – Matana kuelekea mpaka Nyololo, kuna ile barabara ya Nyololo - Kibao, hizi zipewe kipaumbele katika Wilaya ya Mufundi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukienda Kilolo, barabara inayounganisha mkoa na Makao Makuu siku nyingi sana, hata Profesa Msola alikuwa anaisemea sana, haina lami kabisa. Ile inaanzia Ipogolo- Ndiwili- Ihimbo- Luganga- Kilolo, hii nayo ipewe kipaumbele. Pia kuna ile ya Dabaga- Ng‟ang‟ange- Mwatasi- Mufindi, hizi barabara ni za kiuchumi, naomba zipewe kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nizungumzie kuhusu reli ya kati. Mimi nimeolewa na Wasukuma, ni vizuri nikiwazungumzia. Huu ujenzi wa reli ungesaidia sana kuponya barabara zetu, tumekuwa tukitenga pesa nyingi sana kwa ajili ya barabara lakini kama hakuna reli tumekwenda kuona kwenye nchi za wenzetu, nchi nyingi zenye miundombinu mizuri hata uchumi unakwenda kwa haraka sana. Kwa hiyo, ningeomba kwa kweli reli safari hii ipewe kipaumbele cha hali ya juu kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pengine ningetoa tu hata ushauri wangu, pengine kungekuwepo na TANRAIL ambayo itafanya kazi kama TANROADS. Hii TANRAIL ishughulikie tu masuala ya reli, reli ya kati, reli ya TAZARA na ijenge hizi barabara ya Tanga, Tanga mpaka Kigali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, labda niizungumzie kidogo reli ya TAZARA, kwamba, kulikuwa kuna ile sheria ambayo muda mrefu sana tulijua kwamba hii sheria ingeletwa mapema ikabadilishwa tungeweza pia kuwasaidia hii Reli ya TAZARA. Mara ya mwisho Waziri aliyekuwepo alikuwa amefanya mpango kwamba wale Wajumbe wa Miundombinu wangekwenda Zambia wakakutana ili warekebishe hii sheria. Sasa nataka kujua imefikia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo nataka kulizungumzia, ni kuhusu hizi nyumba za Serikali zilizouzwa. Ukisoma kitabu cha Kambi ya Upinzani ukurasa wa tisa unaelezea, lakini nataka kwanza kunukuu kwamba unapozungumzia kitu, nimesoma neno la Mungu kwa sababu Mbunge wangu ni Mchungaji, anasema kwamba toa kwanza boriti kwenye jicho lako ndipo utaona kibanzi kwenye jicho la mwenzio. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimeangalia, hizi nyumba zimeuzwa lini, mwaka 2002, wakati huo Waziri Mkuu alikuwa Mheshimiwa Sumaye na sasa hivi yuko kwenye Kamati Kuu ya CHADEMA. Vile vile nikaona kwamba mgombea wa upinzani naye aliuziwa Plot No. 68 na nikaona kwamba mgombea wa Upinzani, Mheshimiwa Lowassa na yeye pia anahusika. Aliuziwa kwenye 590, sasa ningeomba ushauri huu wangerudisha kwanza wao…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kabati muda wako umekwisha!
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuwapongeza Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea bajeti ili tuweze kuijadili. Yapo mambo ambayo nilikuwa nataka kuishauri Serikali pia na mengine kupatiwa ufafanuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leseni ya makazi, wananchi wengi sana wanaoishi katika maeneo yasiyopimwa Serikali iliweka mpango wa kuwapatia leseni za makazi ili waweze kutumia ardhi yao kupata mikopo ya benki au taasisi mbalimbali za kifedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini muda wa miaka mitatu ni kidogo sana, ni kwa nini Serikali isiweke angalau hata miaka mitano mpaka kumi ili kusiwepo na usumbufu wa mkopaji kama anachukua mkopo wa muda mrefu? Naomba hili liangaliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za pango la nyumba za Shirika la Nyumba. Nimpongeze Waziri mwenye dhamana. Tulishawahi kumsikia katika vyombo vya habari akizungumza kuhusu wananchi wa kipato cha chini kushindwa kumiliki nyumba za kuishi au nyumba za biashara. Kama kweli Serikali inataka na ina dhamira ya kweli ya kuwasaidia wananchi wake ingeangalia upya hizi gharama za pango la nyumba za National Housing kwa sababu wananchi wengi wana kipato cha chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hizi nyumba za gharama nafuu ziangaliwe upya, bei ni kubwa sana, watu wenye kipato cha chini si rahisi kuzinunua. Kama tatizo ni kodi ya vifaa vya ujenzi Serikali ingeondoa ili kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi nchini. Nimpongeze Waziri kwa kuanza kupita katika maeneo yenye migogoro ya ardhi, kwasababu migogoro mingi ni kati ya wakulima na wafugaji, hifadhi na wananchi na mingine ni kati ya wawekezaji na wananchi. Ni kwanini Serikali isiwe na mpango wa kutenga kabisa maeneo kabla ya kuyagawa? Ni kwa nini yasitengwe maeneo ya wakulima ili Serikali iweze kuweka mahitaji yote katika maeneo hayo ili kuondoa hii migogoro? Serikali ina wataalam wa mipango miji, ni kwa nini miji yetu haina mipango? Kumekuwa pia na migogoro hata katika miji yetu sababu wananchi hawajengi majengo kwa mpango. Ni vema Serikali kabla ya kugawa viwanja ingetengeneza mpango mji na baada ya kugawa viwanja basi wasimamie majengo yanayojengwa ili kusiwepo na migogoro ya uvamizi hata ya viwanja vya wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabaraza ya Ardhi. Serikali ilijitahidi kufanya maboresho katika Mabaraza haya ya Ardhi ili mabaraza haya yaweze kutenda haki kwa wananchi. Mara nyingi kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya mabaraza kulalamikiwa kutotenda haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mabaraza haya kumekuwa na changamoto nyingi sana, ni vema Serikali ingeanza kutatua baadhi ya changamoto zinazoyakabili Mabaraza haya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha bajeti yao ili tuweze kuijadili. Yapo mambo ambayo napenda kutoa ushauri na pia kupatiwa ufafanuzi wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini mkakati wa Serikali katika kukuza na kutangaza utalii Kimkoa au Kikanda? Mkoa wetu wa Iringa ni kati ya mikoa ambayo ina vivutio vingi ambavyo kama Serikali ingekuwa na mkakati wa kutosha naamini mkoa wetu ungeweza kuiingizia Serikali pato kubwa sana na pia tungeweza kutengeneza ajira kwa vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Iringa una mbuga ya Ruaha National Park, katika Afrika ni mbuga ya pili kwa ukubwa lakini miundombinu ya barabara ni mibovu sana na bado Serikali haijaweza kuona umuhimu wa kuweka barabara ya lami ili kuvutia watalii wengi kwenda katika mbuga hiyo. Bado Serikali haiwezi kuona umuhimu wa kujenga au kukarabati kiwanja cha ndege cha Nduli, ni vema sasa Serikali ingeweza kuzifanyia upembuzi yakinifu baadhi ya miradi kama ya barabra na viwanja vya ndege ambavyo ni changamoto katika kukuza utalii wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu eneo la Isimila Olduvai Gorge lingeweza kuongeza pato kubwa sana la utalii lakini halitangazwi na halina maboresho kabisa. Mkoa wetu una kaburi na fuvu la kichwa cha Mtwa Mkwawa, bado hakuna matangazo ya kutosha ili tupate utalii wa ndani na nje ya nchi ili tuongeze utalii na vijana wetu kupitia watalii watengeneze ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu TANAPA, shirika hili ni kati ya baadhi ya mashirika na taasisi za umma zinazofanya vizuri sana katika sekta hii ya utalii lakini ni tatizo gani linasababisha Serikali kutokuweka bodi? Mambo mengi na changamoto nyingi zinakosa maamuzi kutokana na shirika kukosa bodi. Ninaomba Mheshimiwa Waziri atakapojibu atoe ufafanuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fidia kwa wananchi wanaoliwa na mamba, kwa kuwa kumekuwa na vifo mara kwa mara kwa wananchi na hasa wanawake wamekuwa wakipata ajali wanapokwenda kufuata maji katika Mto Lukosi katika Wilaya ya Kilolo, Kata ya Ruaha Mbuyuni. Je, ni utaratibu gani unatakiwa kutumika ili wananchi waweze kupatiwa haki zao na je, ni kwa nini wasisaidiwe na Halmashauri kuvuta maji ya bomba katika Mto huo Lukosi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zinazojitokeza katika kutoa vibali vya uvunaji miti msitu wa Taifa wa Sao Hill, kumekuwa na malalamiko makubwa sana ya wananchi katika utoaji wa vibali vya kuvuna miti katika msitu wa Taifa wa Sao Hill. Ninaomba kujua utaratibu unaotumika na Serikali inatambua hilo? Je, ili kuondoa tatizo hilo nini mkakati wa Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Wabunge tumekuwa tukiombwa kuchangia katika taasisi za elimu, afya na hata jamii, je, Serikali ina utaratibu gani wa kuwapatia vibali hivyo vya uvunaji ili kuweza kusaidia jamii na Serikali katika kupunguza changamoto ambazo huwa zinajitokeza wakati tukiwa kwenye ziara za kikazi katika Majimbo na Mikoa kwa ujumla? Ninaomba kupatiwa jibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na pongezi kwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba yao hapa Bungeni ili tuweze kuijadili. Yapo mambo ambayo naomba kupatiwa ufafanuzi wa baadhi ya mambo na mengine kuishauri Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubadilishana wafungwa wa Tanzania na nchi nyingine. Naomba ufafanuzi kama upo uwezekano wa Watanzania ambao wamekwenda nchi nyingine wakapata makosa ya kuhukumiwa kifungo. Je, kuna uwezekano wa wafungwa hao kurudishwa kuja kufungwa hapa nchini au kama kuna uwezekano wa kubadilishana na wafungwa walio hapa nchini kwenda kufungwa katika nchi zao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo napenda kujua kama Watanzania walio nje wakakutwa na makosa, Serikali inawasaidia msaada wa
NAKALA YA MTANDAO (ONLINE DOCUMENT)
221
kisheria sababu najua wengine wanafungwa kwa sababu hawana uwezo wa kuweka mawakili wa kuwatetea, kama nchi msaada gani unatolewa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifo vya Watanzania waishio nje ya nchi: Hivi karibuni yamejitokeza matukio ya mauaji ya kutisha baadhi ya vijana wa Kitanzania wanaishi nchi za nje kama USA kuuawa kwa kupigwa risasi je, ni jitihada gani ambayo Serikali yetu inachukua kubaini hayo? Ningependa kujua jitihada za Serikali kuhusiana na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali kuwaunganisha wajasiriamali wa Tanzania kuingia ubia na makampuni ya China. Serikali ya Awamu ya Tano, sera yake kubwa kufufua na kujenga viwanda kwa ajili ya kujenga uchumi wa nchi na kuongeza ajira na kwa kuwa nchi ya China katika hilo ipo mbali sana ina viwanda vidogo vidogo na vikubwa. Napenda kujua Tanzania imejipanga vipi kuhakikisha inaingia ubia na makampuni ya China yatakayoweza kusaidia ukuaji wa viwanda vyetu nchini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati ya kutembelea Ubalozi wa China na UK. Kwa kweli jengo la Ubalozi wa China lilikuwa lina hali mbaya sana. Je, ni utaratibu gani huwa unatumika katika kupeleka pesa za ukarabati wa majengo hayo kwa sababu ni aibu sana Mabalozi wetu kuishi katika mazingira mabaya na magumu. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na pongezi kwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba yao hapa Bungeni ili tuweze kuijadili. Yapo mambo ambayo naomba kupatiwa ufafanuzi na mengine napenda kuishauri Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubadilishana wafungwa wa Tanzania na nchi nyingine. Naomba ufafanuzi wa kama upo uwezekano wa Watanzania ambao wamekwenda nchi nyingine wakapata makosa ya kuhukumiwa kifungo, je kuna uwezekano wa wafungwa hao kurudishwa kuja kufungwa hapa nchini au kama kuna uwezekano wa kubadilishana na wafungwa walio hapa nchini kwenda kufungwa katika nchi zao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo napenda kujua kama Watanzania waliopo nje ya nchi wakikutwa na makosa, Serikali inawapa msaada wa kisheria, kwa vile najua wengine wanafungwa kwa sababu hawana uwezo wa kuweka Mawakili wa kuwatetea, kama nchi ni msaada gani unatolewa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifo vya Watanzania waishio nje ya nchi; hivi karibuni yamejitokeza matukio ya mauaji ya kutisha baadhi ya vijana wa Kitanzania wanaoishi nchi za nje kama USA kuuawa kwa kupigwa risasi; je, ni jitihada gani ambayo Serikali yetu inachukua kubaini hayo? Ningependa kujua jitihada za Serikali kuhusiana na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali kuwaunganisha wajasiriamali wa Tanzania kuingia ubia na makampuni ya China. Serikali ya Awamu ya Tano, sera yake kubwa kufufua na kujenga viwanda kwa ajili ya kujenga uchumi wa nchi na kuongeza ajira. Kwa kuwa nchi ya China katika hilo ipo mbali sana ina viwanda vidogo vidogo na vikubwa, napenda kujua Tanzania imejipanga vipi kuhakikisha inaingia ubia na makampuni ya China yatakayoweza kusaidia ukuaji wa viwanda vyetu nchini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati ya kutembelea Ubalozi wa Tanzania nchini China na UK, kwa kweli jengo la Ubalozi wa Tanzania China lilikuwa na hali mbaya sana. Je, ni utaratibu gani huwa unatumika katika kupeleka pesa za ukarabati wa majengo hayo kwa sababu ni aibu sana Mabalozi wetu kuishi katika mazingira mabaya na magumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri Profesa Kabudi na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea bajeti yao ili tuweze kuijadili. Kuna mambo ambayo nataka kuyapatia ufafanuzi wake na kushauri pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ucheleweshaji wa kesi za ubakaji; Mkoa wetu wa Iringa ni kati ya mikoa inayokabiliwa na idadi kubwa sana ya kesi ya ubakaji na ulawiti. Inasikitisha sana Bunge lililopita nilileta swali langu hapa Bungeni na niliweza kutoa takwimu ya mwaka 2016 kesi 217 lakini zilizoweza kufikishwa Mahakamani ni kesi 27 tu lakini kila mwaka katika mkoa wetu matukio ya ubakaji yanazidi kuongezeka. Napenda kujua mkakati wa Serikali kuhusiana na jambo hili ni kwa nini kusiwepo na Mahakama Maalum ya kushughulikia kesi hizi. Matukio haya yamekuwa yakiwaathiri watoto wetu kiakili pamoja na mama zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ucheleweshaji wa mabadiliko ya sheria zilizopitwa na wakati; baadhi ya sheria zetu hapa nchini zimekuwa ni za muda mrefu sana na zimepitwa na wakati na kusababisha baadhi ya sheria zetu hapa nchini kutoendana na mabadiliko na kasi ya maendeleo ya Taifa na kuonekana kuwa zimepitwa na wakati. Mara nyingi sana sisi Wabunge tumekuwa tukileta hoja zetu hapa Bungeni lakini bado hatupatiwi majibu ya kuridhisha. Kwa mfano, 12 Aprili, 2017 nilileta swali kuhusiana na Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 lakini bado majibu yake hayaridhishi. Je, ni lini sasa Serikali italeta hoja ya kufanya marekebisho ya kuboresha baadhi ya sheria zilizopitwa na wakati?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufinyu wa bajeti, Wizara hii ni muhimu sana na imekuwa na malalamiko mengi kwa wananchi kutomaliza kesi zao au kuchukua muda mrefu sana. Pia miradi mingi kutokamilika kwa wakati pamoja na bajeti yao kuwa kidogo sana lakini pia pesa yao imekuwa ikicheleweshwa sana na kusababisha miradi kutokamilika kwa wakati hivyo kusababisha miradi hiyo kutumia pesa nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja hii ya Wizara Fedha. Vilevile na mimi nimuunge mkono mjumbe aliyepita kwamba Mheshimiwa Naibu Spika uzi ni huo huo, sheria ni msumeno. Lazima Bunge letu lifuate sheria na kanuni ambazo tumejitungia sisi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze sasa na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wake na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea hii bajeti ili tuweze kuijadili. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais ambaye kwa kweli utumbuaji wake majipu umesaidia sana kuongeza kipato TRA na kwa kweli hakuna mtu ambaye hajui kwamba tumbuatumbua majipu imeweza kutuongezea kipato kikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu naanza na kitabu cha Waziri ukurasa wa 59 kuhusu Shirika la Bima la Taifa (NIC). Kwa kweli nina masikitiko makubwa sana na inaniuma sana. Hili Shirika la Bima lilikuwa shirika ambalo lilisaidia sana nchi hii, wafanyakazi wengi waliweza kuajiriwa, lilikuwa na majengo mengi na mali nyingi sana ambazo leo hii lingeweza pia kuongeza pato kubwa sana katika nchi hii. Hata hivyo, bado Serikali haijawa na mpango haswa wa kuhakikisha kwamba hili shirika linafufuka ili liweze kuwa chanzo kikubwa sana cha mapato katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika bajeti iliyopita ya mwaka 2015/2016, aliyekuwa Waziri wa Fedha alipokuwa anasoma bajeti yake alituambia kwamba Serikali ina mpango wa kuongezea uwezo Shirika la Bima la Taifa kwa Serikali kukatia bima mali zake zote ikiwa ni pamoja na za taasisi na TAMISEMI kupitia shirika hili. Mbona sasa hakuna mpango wowote wa kuhakikisha kwamba haya mashirika yanakatiwa bima katika Shirika hili la Bima? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kuamini mpaka sasa hivi hili shirika halina hata bodi ya wafanyakazi, shirika hili Mkurugenzi wake Mkuu na Wakurugenzi wengi sana wanakaimu tu, sasa kweli hili shirika litajiendeshaje kama bado halijajiwekewa mkakati kama huo? Tuna taasisi karibu 200 katika nchi yetu lakini katika kitabu hiki amesema taasisi 15 tu ndiyo ambazo zinatumia hili Shirika letu la Bima ya Taifa. Niipongeze sana Wizara ya Nishati kwamba imeweza kukata bima katika bomba lake la gesi linalotoka Mtwara mpaka Kinyerezi. Najua ni mapato makubwa sana yanapatikana kwa kukatia bima kwenye Shirika letu la Bima la Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua siku zote huwa tunawasifia Wachina wanaongeza pato na sisi tulienda kweli tukaona Wachina jinsi walivyokuwa wazalendo. Kama nchi hii haitakuwa na uzalendo mashirika yetu mengi sana yatakufa. Kwa sababu ipo TTCL, Posta bado hatutumii mashirika yetu vizuri, tunaona mashirika na taasisi za Serikali zinaenda kukata bima sehemu nyingine. Unaona tu Wachina wamekuja hapa wamewekeza lakini wameleta pia mashirika yao ya bima, wameleta pia walinzi wao, wameleta kila kitu mpaka wafagiaji. Lazima iwepo sheria kwamba haya mashirika yetu ya bima yatumike pia ili kuongeza Pato la Taifa letu. Nitamuomba Waziri atakapokuwa anajibu angalau atupe mkakati kwamba ana mkakati gani wa kuyafufua haya mashirika na ni kwa nini mpaka leo hii hakuna hata bodi ya wafanyakazi kwenye hili shirika na Wakurugenzi bado wanaendelea kukaimu siku zote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi pia niendelee kuunga mkono kuhusiana na ile Sheria ya Manunuzi ya mwaka 2011. Wabunge wengi sana siyo leo tu, siku zote tumekuwa tukiisema hii sharia, kwa nini hailetwi, kuna kitu gani kimejificha hapa nyuma? Kwa sababu hii sheria ingeletwa leo hii tusingekuwa tunalalamika, hii sheria ndiyo mkombozi. Naomba Mheshimiwa Waziri atujibu, tulipewa matumaini kwamba katika Bunge hili hii sheria ingekuja tungeweza kuibadilisha, mbona hakuna chochote, kuna tatizo gani katika uletaji wa hii sheria hapa Bungeni?
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusu VICOBA, hakuna siri VICOBA ni mkombozi wa sisi wananchi hasa wanawake. VICOBA hii imetufichia mambo mengi sana, wanawake walikuwa wanadhalilika sana kwenye taasisi nyingine za fedha kwa kuchukuliwa mali zao lakini VICOBA imekuwa kama ndiyo mkombozi. Tuliambiwa kwamba VICOBA inaendeshwa bila kusimamiwa na sheria yoyote ya fedha na tuliambiwa sheria ingeletwa hapa ili tuweze kuipitisha lakini hakuna sheria iliyoletwa mpaka leo. Sasa wanatuambia nini kuhusiana na VICOBA kuendeshwa bila sheria yoyote ya fedha? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusu malipo ya wazabuni. Wazabuni wetu wanapata shida sana, ningeomba kujua ni lini Serikali italipa malipo wazabuni wanaozidai kwa muda mrefu sana Halmashauri na Wizara zetu. Wamekuwa wakizungushwa mno, wanaambiwa kwamba malipo yao yapo Hazina lakini wakienda Hazina bado hawalipwi, lakini hao wazabuni bado pia wanadaiwa kodi za Serikali. Sasa tutakusanyaje kodi kama hatuwalipi hawa wazabuni, watafanyaje biashara? Hawa wazabuni wamekuwa wakichukua mikopo kwenye benki, wanadaiwa riba, halafu TRA bado wanawatoza tena kwa nini wamechelewesha kulipa kodi zao. Serikali hii imesema kwamba itawasaidia wafanyabiashara wadogo wadogo na wa kati, huko ndiyo kuwasaidia wazabuni? Kwa sababu wazabuni walio wengi ndiyo ambao wanatoa zabuni kwenye Halmashauri zetu na kwenye Wizara zetu. Ningeomba kwa kweli uwepo mkakati wa kushughulikia suala hili kwa sababu ni muda mrefu sana wazabuni wamekuwa wakipata matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kuzungumzia kuhusu ucheleweshaji wa pesa za miradi katika Halmashauri na Wizara zetu. Huu ucheleweshaji siyo wa mara moja, siku zote pesa za maendeleo ya miradi zimekuwa zikicheleweshwa sana na ucheleweshaji huu wa miradi umekuwa ukisababisha miradi ile sasa inafanyika kwa gharama kubwa sana. Kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Iringa kuna ule mradi wa machinjio wa kisasa, ulitakiwa tuujenge kwa pesa kidogo sana, lakini kadri fedha ambavyo zinacheleweshwa kuletwa ule mradi pia gharama zake zinaongezeka. Pia ule mradi kama tungekuwa tumeumaliza kwa wakati ungeweza kusaidia chanzo kikubwa cha mapato kwa sababu tunategemea kwamba tutapata mapato hata ya dola kwa sababu tutasafirisha zile ngozi nje ya nchi.
Vilevile tulikuwa tunategemea kuajiri wafanyakazi wengi sana katika Halmashauri yetu kupitia mradi ule. Sasa utaratibu gani huwa unatumika, ni kwa nini hizi pesa za miradi zinacheleweshwa sana? Karibu sehemu zote watu wanalalamika ucheleweshaji wa pesa katika miradi ya Halmashauri zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi sana wamezungumzia kuhusu riba kubwa inayotozwa na baadhi ya taasisi za fedha. Taasisi nyingi sana zimekuwa zikitoza riba kubwa sana na wananchi wengi sana wanashindwa kufanya biashara.
Wananchi wengi sana sasa hivi wakichukua mikopo benki mali zao zinauzwa, imesababisha wananchi wengi sana kupoteza maisha au kupata hata pressure kwa sababu mikopo halipiki dhamana zinachukuliwa. Ukichukua sasa hivi mkopo benki ujue kwamba wewe umeajiriwa na benki hupati chochote zaidi tu utafanya ile kazi, kama umechukua kwa ajili labda ya uzabuni basi utafanya kazi ya uzabuni, zabuni yenyewe wanakusumbua.
Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie upya hizi riba ambazo mabenki yetu yamekuwa yakitoza, ikae na ione ni kiasi gani ambacho kinaweza kikasaidia. Kwa sababu biashara ni ngumu sana, watu wanatozwa katika majengo, kuna tozo nyingi mno ambazo ukienda kuchukua mkopo unaona riba imekuwa kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie kuhusu hizi mashine za EFDs. Wengi wamezungumzia suala hili, tulitegemea kwamba hizi mashine zingekuwa mkombozi, tungekusanya kodi nyingi sana. Tatizo utaona labda mtu mmoja au wawili ndiyo wana zile mashine wengine hawatumii, kwa hiyo, wengine wanalipa kodi wengine hawalipi, naomba hili suala liangaliwe. Pia Serikali ilisema ingetoa hizi mashine bure sijui zoezi hili limefikia wapi, ningependa kujua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri na hasa ya ziara zake mikoani na busara anazozitumia katika utatuzi wa changomoto mbalimbali. Pia niwapongeze Mawaziri Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Antony Mavunde na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nianze mchango kwa mambo yafuatayo; ucheleweshaji wa pesa za maendeleo katika miradi ya maendeleo. Kutokana na pesa za miradi kucheleweshwa katika Halmashauri zetu kunasababisha miradi mingi kutokamilika kwa wakati na pia kuongezeka kwa gharama za miradi variation.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Manispaa yetu ya Iringa iliyopo katika Jimbo la Iringa Mjini kuna mradi wa machinjio ya Ngerewala. Mradi huu mzuri lakini umeanza toka mwaka 2007. Mradi huu ukikamilika ungeweza kutoa ajira kwa wananchi wa Iringa zaidi ya 200.
Mheshimwa Spika, nashauri ni vema Serikali ingetoa pesa katika mradi huu kiasi cha shilingi bilioni moja ili Halmashauri isiingie kwenye mkataba mbovu wa miaka 25. Pia atafutwe mtaalam mshauri ili asaidie mradi huu uendeshwe kwa faida kwa sababu hiki ni chanzo kizuri sana
cha mapato. Mfadhili akipata atapandisha bei ya uchinjaji na kusababisha wachinjaji kuchinjia mtaani na inaweza pia kusababisha bei ya nyama kupanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mifuko ya Jamii, nipongeze jitihada zinaofanywa na mifuko ya jamii ya NSSF, LAPF, PPF, GEPF, PSPF na NHIF kwa kukubali wito wa kuanza kujenga viwanda ikiwemo ufufuaji wa kinu cha kusaga mahindi. Lakini niiombe Serikali iweze kulipa madeni inayodaiwa na mifuko hiyo ili viwanda vijengwe ambavyo vitasaidia kukuza uchumi na kuongeza ajira nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fao la kujitoa, pamoja na nia nzuri ya Serikali ya kujali wafanyakazi pale wanapostaafu au wanapoacha kazi, lakini sheria ya kuzuia wafanyakazi kujitoa kwenye mifuko pale ajira zao zinapokomaa hadi mfanyakazi atimize miaka 60 hili ni tatizo kubwa sana kwa sababu ajira za wafanyakazi zimetofautiana. Mfano sekta ya ujenzi, sekta ya kilimo na sekta ya kazi za majumbani si rahisi wafanyakazi wa sekta hizo kufikisha miaka 60 tunashauri sheria hiyo itofautishe sekta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la watu wenye ulemavu, niipongeze Serikali kwa kuwatambua watu wenye ulemavu nchini lakini bado wanachangamoto hasa katika suala la usafiri, bado vyombo vya usafiri sio rafiki, ni lini Serikali italiangalia hili? Pia ni kwa nini katika ile mikopo ya Halmashauri na wao wasitambulike kutengewa asilimia zao katika asilimia tano ya vijana na akina mama? Walemavu wengi ni wajasiriamali lakini hawakopeshwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamezungumza kuhusu kumtua ndoo kichwani mwanamke. Katika Mkoa wetu wa Iringa limekuwa ni tatizo kubwa sana hasa katika maeneo ya vijijini. Kinachosikitisha Serikali imekuwa ikitumia pesa nyingi sana kwa miradi ya maji lakini maji hayatoki
kama miradi ya Ilindi, Ng’uruhe, Ihimbo, Iparamwa Ruaha Mbuyuni na Mkosi. Lakini mkoa wetu una Mto Ruaha, Lukosi na Mtitu na chanzo cha Mto Mgombezi. Ni kwa nini mito hii isitumike katika kusambaza maji kuliko hiyo miradi ya visima iliyotengwa. Je, Serikali inawachukulia hatua gani hawa? Mheshimiwa Mwenyekiti, Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango wangu niliochangia kwa kuongea, napenda pia niongeze mchango wangu kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia magari ya zimamoto katika viwanja vya ndege. Viwanja vingi vina changamoto kubwa sana ya magari ya kuzima moto kikiwepo na Kiwanja cha Nduli, Mkoa wa Iringa. Gari lililoletwa Mkoa wa Iringa lilitokea Kiwanja cha Tabora likiwa bovu na halijawahi kufanya kazi toka limeletwa. Hivyo kiwanja hakina gari la kuzimia moto, gari linalotumika ni la Ofisi ya Zimamoto kama kukiwa na ugeni wa viongozi na sasa hivi gari lile limepata ajali. Napenda kufahamishwa utaratibu unaotumika kupeleka haya magari katika viwanja au kama kuna vigezo vinavyotumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nizungumzie TCRA na mtambo wa TTMS. Nashukuru sana kwa uongozi wa TCRA kwa kutupatia semina ya uelewa wa taasisi yao ikiwemo na matumizi ya huu mtambo wa TTMS. Pamoja na huu mtambo kuwa ndiyo mtambuzi wa namna bora ya kupata taarifa za makusanyo ya makampuni ya simu ili Serikali iweze kutoza kodi stahiki kutokana na miamala ya fedha inayofanyika kupitia simu za mikononi, je, ni lini sasa ule mfumo wa Revenue Assurance Management System (RAMS) utafungwa? Tulipotembelea TCRA tuliambiwa kuwa wana mazungumzo na mkandarasi, nini mkakati wa Serikali kuhusiana na hilo? Napenda kujua kuhusu suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, niongelee kuhusu madeni ya TTCL. Pamoja na Serikali kumiliki hisa kwa 100% lakini bado shirika hili linatakiwa liendelee kujiendesha. Je, ni lini Serikali itaweka mkakati wa kuhakikisha madeni yote yanalipwa, sababu imeamua kulipa madeni yake? Wizara zote zilishafanya uhakiki wa madai, je, haya madeni ya TTCL Wizara wameshaanza kulipa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ni Internet Data Center. Niipongeza Serikali kwa ujenzi wa kituo hiki kwa ajili ya kutunza na kuhifadhi kumbukumbu. Hata hivyo, ukiangalia katika bajeti zetu kuna baadhi ya Wizara na Taasisi za Serikali pia zinatenga bajeti kwa ajili ya kuwa na data center zao. Je, ni kwa nini kituo hiki kisitumike kwa taasisi zote za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, ni TAZARA. Nataka kujua ni lini ule upungufu wa ile Sheria Na. 23 ya mwaka 1975 kama ilivyofanyiwa marekebisho na Sheria Na. 4 ya mwaka 1995 itafanyiwa marekebisho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara hii. Kwanza kabisa nianze kutoa pongezi zangu kwa kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Naibu Waziri Engineer Ngonyani, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa taasisi zote katika Wizara hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, na mimi kwa kweli kwa sababu ni Mjumbe wa Kamati ya Miundombinu nianze kupongeza kazi nzuri ambazo zimefanywa na Serikali ya Awamu hii ya Tano kama vile ujenzi wa Daraja la Kigamboni, ujenzi wa mabweni UDSM, uzinduzi wa ujenzi wa reli ya kati, uzinduzi wa miradi ya flyovers, TAZARA na Ubungo, Serikali kumiliki asilimia 100 TTCL, mradi wa ujenzi wa upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam na ununuzi wa ndege ya ATCL na kubwa kuliko zote, Serikali kuanza kulipa wakandarasi na washauri shilingi bilioni 788 kutoka katika deni la shilingi bilioni 930.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali hili zoezi liwe endelevu ili miradi yetu ikamilike kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuzungumzia kuhusu ujenzi wa viwanja vya ndege. Naipongeza Serikali kuendelea na ujenzi wa viwanja vya ndege kote nchini, ni pamoja na jengo lile la abiria Terminal III Kiwanja cha Mwalimu Nyerere.
Mheshimiwa Naibu Spika, japokuwa tulipotembelea tulikuta kuna changamoto ya pesa kutopelekwa kwa wakati, sasa naiomba Serikali ipeleke pesa kwa wakati ili jengo liweze kukamilika na liendane na ununuzi wa ndege zetu. (Makofi)
Niendelee kupongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kutenga pesa kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja chetu cha Nduli. Hiki kiwanja kwa kweli tumekuwa tukikidai kwa muda mrefu, sasa tunaishukuru Serikali angalau imeweza kutenga pesa na sisi kiwanja chetu cha Nduli sasa kitajengwa na najua hata Bombardier sasa itatua pale. Nitoe tu ushauri, kwamba pamoja na kuwa huu mradi tayari wananchi wa pale wameshaukubali sasa waweke alama katika yale maeneo ambayo upanuzi utafanyika ili yale maeneo yasiweze kuendelezwa, kwa sababu yakiendelezwa wakati wa kulipa fidia itakuwa tatizo kubwa sana.
Vilevile niiombe Serikali sasa, kuna viwanja vingi sana havina hati miliki kikiwemo hiki cha Iringa. Kwa hiyo, sasa itengeneze hati ili wananchi wasiendelee kuvamia katika hivi viwanja vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee na ujenzi wa barabara nchini. Niipongeze sana Serikali kwa kuendelea na ujenzi wa miradi ya barabara kwa kiwango cha lami.
Naomba niunge mkono ushauri, Mheshimiwa Serukamba alipokuwa akichangia amesema kwamba angalau zile barabara za Wilaya TANROADS iendelee kuzihudumia, kwa sababu tunaona hata sisi wenyewe tulipokuwa tunachangia watu wengi sana wanalalamikia barabara zilizopo katika vijiji kwamba miradi haiendi kwa wakati na vilevile tumeona kwamba hakuna wataalam wengi kwenye Halmashauri zetu. Kwa hiyo, kama barabara hizi zitamilikiwa na TANROADS tuna imani kabisa zitakwenda vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia labda uwepo upembuzi yakinifu katika miradi ya barabara zetu, kwamba zile za kiuchumi ziweze kupewa kipaumbele, kwa sababu tumekuwa na barabara nyingi za kiuchumi katika halmashauri zetu ambazo zinakuwa hazijengwi kwa kiwango cha lami kiasi kwamba sasa wakati wa mvua malori yanakwama. Kwa mfano pale Iringa tuna miti, kama Mgololo kule unaona wakati wa mvua malori yanakwama na kuna ajali nyingi sana zinatokea.heshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile ubovu huu wa barabara hasa vijijini unasababisha hata vifo vya akina mama na watoto. Kwa sababu ya miundombinu ambayo ipo katika barabara zetu zilizopo vijijini wakati wa mvua akina mama wengi hawafikiwi. Kwa hiyo, mimi niombe hizi barabara zipewe kipaumbele ili kupunguza pia vifo vya akina mama na watoto katika vijiji vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie pia barabara zilizopo katika Mkoa wetu wa Iringa. Tunashukuru sana Serikali katika bajeti hii imeweza kutenga pesa kuanza ujenzi wa barabara inayokwenda katika mbuga ya Ruaha. Muda mrefu sana tumekuwa tukiizungumzia barabara hii kwa sababu utalii utaongezeka katika mkoa wetu na mikoa iliyopo katika Nyanda za Juu Kusini. Kwa hiyo, mimi nishukuru kwamba japo kuwa wametenga pesa, lakini sasa ujenzi ufanyike kwa sababu kutenga pesa ni kitu kingine na kuanza ujenzi ni kitu kingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo barabara za kiuchumi kama barabara ya Mafinga – Mgololo, Kinyanambo
– Isalavanu – Saadani – Rujewa, kuna Kiponzelo – Wasa, kuna barabara ile ya Kilolo mpaka Iringa Mjini. Tunaomba Serikali yetu izipe kupaumbele kwa sababu uchumi wa mkoa wetu unazitegemea sana hizi barabara ambazo ziko katika wilaya hizo nilizozitaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie watu wenye ulemavu. Sisi wote hapa ndani ni walemavu watarajiwa. Nilipoongea na watu wenye ulemavu katika Mkoa wangu wa Iringa yapo mambo ambayo wanalalamikia hasa miundombinu katika magari. Inaonekana kwamba watu wengi wenye ulemavu bado Serikali haijawaangalia. Watu wanakuwa na baiskeli lakini hawawezi kupandisha kwenye gari kwa sababu hakuna miundombinu inayoruhusu mtu mwenye ulemavu kuweka baiskeli yake kwenye gari lolote.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile majengo yetu bado si rafiki sana na watu wenye ulemavu kiasi kwamba yanasababisha hawa watu wenye ulemavu kukosa hata huduma nyingine. Utakuta mama mwenye ulemavu ni mjamzito anashindwa kupandisha ngazi kwenda kumuona daktari. Kwa hiyo, mimi ningeomba sheria iwepo ili watu wenye ulemavu pia wazingatiwe wakati wanajenga haya majengo yote yakiwepo hata majengo ya shule zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile TCRA labda iangalie, pia hata katika televisheni zetu bado hawajaweka watu kutafsiriwa zile lugha za watu wenye ulemavu. Kwa hiyo mambo yote hayo yazingatiwe. Hakuna pia michoro kwenye barabara kuonesha watu wenye ulemavu wanapopita, kwa hiyo mimi naomba haya mambo yazingatiwe kwa sababu sisi wote ni walemavu watarajiwa, huwezi kujua wewe lini utakuwa mlemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuzungumzia kuhusu Shirika la Posta Tanzania. Kwa sababu Serikali imeanza kuyafufua mashirika nchini, ni kwa nini sasa Serikali isitoe mtaji wa kutosha ili hili shirika liweze kujiendesha. Shirika hili lilikuwa na deni kama la shilingi bilioni 5.1 ambapo Serikali imelipa shilingi bilioni 2.5 tu kwa shirika.
Sasa mimi ningeomba sasa hivi hili shirika lizingatiwe kwa sababu lilikuwa lina mali nyingi sana hapo zamani. Kwa hiyo mimi naomba wapatiwe pesa zao zilizobaki ili na lenyewe liweze kujiendesha ili wafanyakazi wale pia waweze kufanya kazi kwa kujiamini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nizungumzie mradi wa postal code na symbol za posta. Huu mradi kwa kweli umekuwa mara nyingi sana; kwanza ni muhimu sana kwa sasa hivi kwa sababu kwanza makazi yatatambulika, na isitoshe hatakukusanya kodi tutakusanya kwa urahisi kama nyumba zitakuwa zinatambulika kutokana na hizi symbol za posta, lakini mara nyingi sana imekuwa ikitengewa pesa kidogo sana kila mwaka, mimi naomba safari hii…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kuunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri Mheshimiwa Kigwangalla na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba yao hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya ni moja ya sekta nyeti Tanzania inayosimamiwa na Wizara ya Afya pamoja na hospitali zote za rufaa, hospitali za wilaya pamoja na vituo vya afya na zahanati zilizopo chini ya Serikali za Mitaa, Manispaa na Wilaya hizi zipo chini ya Wizara ya TAMSEMI, pamoja na kwamba zote zinapatiwa miongozo ya kiutendaji kutoka Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na umuhimu wa Idara ya Afya katika Mkoa wetu wa Iringa, inakabiliwa na changamoto zifuatazo:-

i) Chumba cha uangalizi wa wagonjwa wa nje wa dharura (OPD) hivyo kusababisha msongamano mkubwa katika wodi kwa zile huduma zinazohitajika uangalizi wa muda mfupi.

(ii) Wastani mdogo wa daktari kwa wagonjwa. Hivyo kufanya kuwa na msongomano mkubwa katika vyumba vya madaktari wachache wanapokuwa zamu, hivyo kuongeza work load kwa madaktari.

(iii) Kuna wodi nzuri za watoto zilizojengwa kwa ufadhili wa Hospitali ya Vicensa ya Italy na mzalendo mmoja familia ya ASAS lakini hakuna Daktari Bingwa wa Watoto (Pediatrician) pamoja na idadi kubwa ya watoto wanaolazwa hospitalini hapo.

(iv) Hakuna kitengo cha ENT (sikio, pua na koo) wala Daktari wa ENT. Hivyo case zote za ENT lazima zipewe rufaa au kusubiri visiting doctor ambayo inakuwa ni kero kwa wagonjwa wenye matatizo yanayohusiana na tatizo hilo.

(v) Vitendea kazi muhimu wodini ni vichache kama vile oxygen cylinder na oxgen concentrators, pulsonetor za kupima kiwango cha oxygen kwa mgonjwa, BP machine hazina uwiano inaostahili kwa ugonjwa (wodi nzima inakuwa na mashine moja tu), vipimo vya sukari kwa wagonjwa wa sukari waliopo wodini wanaohitaji uangalizi wa kina.

(vi) Kitengo cha afya ya akili hakikidhi haja na mahitaji ya wagonjwa wa afya ya akili kwa sababu kina vyumba vinne yaani viwili kwa wanaume na viwili kwa wanawake, vyenye uwezo wa kukaa na wagonjwa wawili kila chumba, hivyo uwezo wa hospitali kuhudumia wagonjwa wa akili ni wagonjwa wanne tu, ambavyo ni hatari kwa hospitali yenye kiwango cha Hospitali ya Mkoa ya Rufaa ukizingatia Mkoa.

(vii) Wagonjwa wanaostahili msamaha hawapati huduma za dawa kama inavyostahili kutokana dawa nyingi kutokuwepo hospitalini, hivyo kusababisha shida zaidi kwa wagonjwa wasio na uwezo, wazee na wenye magonjwa ya kudumu kama sukari, akili, TB na HIV.

(viii) Nyumba za madaktari zaidi ya asilimia 85 ya madaktari na wahudumu wengine wa afya wanakaa maeneo ya mbali na hospitali kutokana na kukosekana nyumba hasa nyakati za usiku kwa wagonjwa wetu.

(ix) Kukosekana kwa huduma zingine za msingi kama CT Scan, MRI, ECG, ECHO katika hospitali ya Mkoa hivyo kusababisha rufaa zingine zisizokuwa na lazima ambapo ni kero kwa wananchi wanaohitaji huduma hizo.

(x) Mifumo ya ki-eletronic inayowezesha daktari kupata majibu ya mgonjwa kutoka maabara na taarifa nyingine za mgonjwa kwa haraka kama ilivyo hospitali nyingine za private.

(xi) Pia dawa muhimu hazipo hospitalini kila wakati, hivyo kusababisha wagonjwa kuhangaika kwenda kutafuta maduka binafsi na kero zaidi inakuwa wakati wa usiku ambapo hayo maduka binafsi yamefungwa, inaweza kuhatarisha maisha ya mgonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Benki ya Wanawake; niipongeze Serikali kwa kuweka dirisha la kuweza kuhudumia wananchi wa Mkoa wa Iringa, lakini ili ile dhamira ya kuanzisha benki hii kwa ajili ya wanawake ipate kutimia. Pia kuwepo na mobile agency kwa ajili ya huduma hii kufikishwa vijijini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vituo vinavyolea watoto yatima; pamoja na wamiliki wa vituo hivi vya watoto yatima kuisaidia Serikali katika wimbi hili la watoto yatima na watoto wa mtaani, lakini kuna changamoto nyingi zilizopo katika vituo hivi. Kuna vituo havina hata uwezo wa kuwatibu watoto hawa wanapougua au kupata ajali. Hivyo ni vema Serikali ikaweka utaratibu wa kusaidia vituo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Dkt. Harrison Mwakyembe Waziri, Naibu Waziri Anastazia Wambura, Makatibu Wakuu na watendaji wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba hapa Bungeni ili tuijadili. Yapo mambo ambayo nahitaji kuyachangia ambayo ni:

Moja, ufinyu wa Bajeti; siku zote Wizara hii imekuwa ikipatiwa bajeti finyu sana na kusababisha Wizara hii kufanya kazi zake katika wakati mgumu sana na mbaya zaidi pamoja na kupatiwa bajeti kidogo lakini hata bajeti iliyopangwa haipelekwi kwa wakati hivyo kusababisha Miradi mingi iliyopangwa kutokamilika kwa wakati. Ni vema Wizara hii ingepewa kipaumbele kwa sababu pia imekuwa ikifanya kazi ya vijana wetu inayohusiana na sanaa.

Mheshimiwa Spika, uvamizi wa viwanja vya michezo katika Halmashauri, vijana wetu wanakosa haki yao ya msingi kutokana na uvamizi uliofanywa katika viwanja vilivyoachwa wazi kwa ajili ya michezo kuvamiwa na kugawiwa kwa watu kujenga. Nakumbuka Serikali ilitoa tamko kuwa waliovamia viwanja vya wazi waondolewe lakini mpaka leo hakuna hatua zozote zilizochukuliwa na Serikali kwa ajili ya jambo hilo. Hivyo, ningependa kupatiwa ufafanuzi wa agizo hilo la Serikali sababu vijana wengi hawana maeneo ya michezo.

Mheshimiwa Spika, Vazi la Taifa; ningependa kujua mpango wa Serikali kuhusiana na vazi la Taifa, nakumbuka Serikali ya Awamu ya Nne ilishawahi kutuletea taarifa kuhusiana na mchakato wa kupata vazi hilo lakini mwisho wake mpaka leo hatujui limefikia wapi.

Mheshimiwa Spika, (TBC) Shirika la Utangazaji la Taifa; naomba Serikali ifanye jitihada za kutosha kuhakikisha TBC inapatiwa pesa ya kutosha ili iweze kusikika nchi nzima. Tunasikia vibaya kuona maeneo ya mipakani wanapata mawasiliano toka nchi jirani. Pia vitendea kazi viboreshwe viendane na hadhi ya chombo cha Serikali.

Mheshimiwa Spika, watu wenye ulemavu; naomba Serikali iwatendee haki watu wenye ulemavu kwa kuweka Sheria ya kuhakikisha wamiliki wote wenye Television wanaweka watafsiri wa lugha katika Television ili watu wenye ulemavu wa kusikia nao waweze kuona. Pia itawasaidia kupata ajira kwa watu waliosomea kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, michezo ya UMISETA; naiomba Serikali yetu iweke kipaumbele kikubwa sana katika kutenga pesa kwa ajili ya michezo hiyo ili tuweze kuibua vipaji vya watoto wetu ili tuviendeleze kwa ajili ya kusaidia nchi hii kwa upande wa maendeleo ya michezo. Michezo ni ajira, michezo ni afya na michezo inajenga mahusiano.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Ummy Mwalimu; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha vizuri hotuba yao hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya ni moja kati ya sekta nyeti Tanzania inayosimamiwa na Wizara ya Afya pamoja na hospitali zote za rufaa, hospitali za wilaya pamoja na vituo vya afya na zahanati zilizopo chini ya Serikali za Mitaa (Manispaa na Mitaa). Hizi zipo chini ya Wizara ya TAMISEMI pamoja na kwamba zote zinapata miongozo ya kiutendaji kutoka Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na umuhimu wa Idara hii ya Afya, Mkoa wetu wa Iringa unakabiliwa na changamoto zifuatazo:-

(i) Kukosekana kwa chumba cha uangalizi wa wagonjwa wa nje wa dharura OPD (Casuality/Emergence) hivyo kusababisha msongamano mkubwa wodini kwa zile huduma zinazohitaji uangalizi wa muda mfupi;

(ii) Uwiano mdogo wa daktari kwa mgonjwa, hivyo kufanya kuwa na msongamano mkubwa katika vyumba vya Madaktari wachache wanaokuwa zamu na kuongeza workload kwa Madaktari;

(iii) Kuna wodi nzuri za watoto zilizojengwa kwa ufadhili wa Hospitali ya Vicensa ya Italia na mzalendo mmoja, familia ya ASAS, lakini hakuna Daktari Bingwa wa watoto (pediatrician) pamoja na idadi kubwa ya watoto wanaolazwa hospitalini hapo;

(iv) Hakuna Kitengo cha ENT (sikio, pua na koo) wala Daktari wa ENT hivyo, case zote za ENT lazima zipewe rufaa au kusubiri visiting doctor ambapo ni kero kwa wagonjwa wenye matatizo hayo;

(v) Vitendea kazi muhimu wodini ni vichache kama vile oxygen cylinder na oxygen concentrators, pulsometor za kupimia kiwango cha oxygen kwa wagonjwa, BP machines hazina uwiano unaostahili kwa ugonjwa (wodi nzima inaweza kuwa na mashine moja tu) na vipimo vya sukari kwa wagonjwa wa sukari waliopo wodini wanaohitaji uangalizi wa kina;

(vi) Kitengo cha Afya ya Akili hakikidhi haja na mahitaji ya wagonjwa wa afya ya akili kwa sababu kina vyumba vinne yaani viwili kwa wanaume na viwili kwa wanawake vyenye uwezo wa kukaa na wagonjwa wawili kila chumba. Hivyo, uwezo wa hospitali kuhudumia wagonjwa wa akili ni wagonjwa nane tu ambayo ni hatari kwa hospitali yenye kiwango cha Hospitali ya Mkoa ya Rufaa;

(vii) Wagonjwa wanaohitaji msamaha hawapati huduma za dawa kama inavyostahili kutokana na dawa nyingi kutokuwepo hospitalini. Hali hii husababisha shida zaidi kwa wagonjwa wasio na uwezo, wazee na wenye magonjwa ya kudumu (sukari, akili, TB na HIV);

(viii) Nyumba za Madaktari, zaidi ya 85% ya Madaktari na wahudumu wengine wa afya wanakaa maeneo ya mbali na hospitali kutokana na kukosekana nyumba. Hii ni changamoto hasa inapohitajika huduma ya dharura kwa mgonjwa hasa nyakati za usiku;

(ix) Kukosekana kwa huduma nyingine za msingi kama CT Scan, MRI, ECG, ECHO katika Hospitali ya Mkoa na kusababisha rufaa nyingine zisizokuwa na lazima ambapo ni kero kwa wananchi wanaohitaji huduma hizo;

(x) Kukosekana kwa mifumo ya kielektroniki inayowezesha daktari kupata majibu ya mgonjwa kutoka maabara na taarifa nyingine za mgonjwa kwa haraka kama ilivyo hospitali nyingine za private;

(xi) Kila wakati kukosekana kwa dawa muhimu hospitalini na kusababisha wagonjwa kuhangaika kwenda kutafuta dawa kwenye maduka ya watu binafsi na kero zaidi inakuwa wakati wa usiku ambapo na hayo maduka binafsi yanapokuwa yamefungwa, inaweza kuhatarisha maisha ya mgonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu Benki ya Wanawake. Niipongeze Serikali kwa kuweka dirisha la kuweza kuhudumia wananchi wa Mkoa wa Iringa. Hata hivyo, niiombe Serikali itoe mtaji wa kutosha ili ile dhamira ya kusaidia benki hii kwa ajili ya wanawake ipate kutimia. Pia nashauri kuwepo na mobile agency kwa ajili ya huduma hii kufikishwa mpaka vijijini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu vituo vinavyolelea watoto yatima. Pamoja na wamiliki wa vituo hivi vya watoto yatima kuisaidia Serikali katika wimbi hili la watoto yatima na watoto wa mtaani lakini kuna changamoto nyingi zilizopo katika vituo hivi, kuna vituo havina hata uwezo wa kuwatibu watoto hawa wanapougua au kupata ajali. Hivyo, ni vema Serikali ikaweka utaratibu wa kusaidia vituo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Maghembe, Naibu Waziri, Engineer Ramo Makani, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea bajeti yao ili tuweze kuijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Wanyama ya Ruaha National Park ni hifadhi ya pili kwa ukubwa katika Afrika na hifadhi yenye wanyama wengi sana. Cha kushangaza hifadhi hii barabara inayoenda katika mbuga hii haina lami na kiwanja cha ndege cha Iringa hakuna ndege kubwa inayotua katika kiwanja hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijajua Wizara hii inafanya juhudi gani kuhakikisha miundombinu ya kuwezesha watalii wanaofika na kufanya matangazo ya kutosha ili tupate watalii wa kutosha? Ni kwa nini Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, Serikali haiwekezi kama ilivyo Kaskazini? Kwani kuna vivutio vingi sana. Ni vizuri Serikali ingetupatia mkakati wa kuendeleza mbunga hiyo na utalii wa Nyanda za Juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kitabu kilichotolewa na TFS kilichotoa mwongozo wa kutoa vibali, tunashukuru kwa kutangulia kutoa kipaumbele kwa wenye viwanda na wananchi watakaozunguka msitu; lakini nitoe ushauri wangu kwa Serikali kuwa katika mwongozo wake ungeongeza na yale makundi maalum; makundi ya akina mama wajane, akina mama wenye vyama vinashughulikia makundi ya kijamii. Kwa sababu tumeshuhudia mara nyingi wananchi wanaozunguka msitu hawafaidiki na rasilimali hiyo, wakati wao ndio walinzi wakuu wa mazingira hayo, hata wakati mwingine moto ukitokea wanakuwa wakitoa msaada mkubwa. Naiomba Serikali jambo hilo liangaliwe tena na tupatiwe majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie upya suala la fidia kwa wananchi wanaopatwa na maafa. Kwa mfano, Mkoa wa Iringa kuna wananchi walipata matatizo ya kuuawa na mamba wengine kupata ulemavu.

Pia tembo walileta uharibifu wa mali na vifo katika Kata ya Nyanzwa, lakini tunashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri Engineer Ramo alishawahi kufanya ziara katika eneo hilo na kilio kikubwa kilikuwa ni fidia kidogo sana ukilinganisha na uharibifu unaojitokeza. Ni vigezo gani huwa vinatumika au ni lini sheria itarekebishwa ili ianze kukidhi vigezo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa una vivutio vingi sana ambavyo bado hatuoni kama Serikali inavitendea haki ya kuvitangaza ili viweze kuchangia pato na kukuza utalii katika eneo la Nyanda za Juu Kusini. Tunaona kama upo ubaguzi. Nini mkakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Nabu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba hii ambayo ni muhimu sana kwa sisi akina mama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Mawaziri wake ambao wako katika Wizara hii. Vilevile nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia ambaye alikuja Iringa kwa ajili ya kukagua vyanzo vya maji. Niiombe tu Serikali iangalie yale maagizo aliyoyatoa siku zile alivyokuwa Iringa basi yazingatiwe. Tuna imani kwamba kama yatazingatiwa angalau Iringa na sisi vile vyanzo vinaweza vikawasaidia wanawake wa Iringa na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niunge mkono Wabunge wote waliochangia kuhusu Mfuko ule wa Maji uongezewe kutoka kwenye shilingi 50 mpaka shilingi 100. Nina imani kabisa ili mwanamke atuliwe ndoo kichwani ni muhimu mfuko huu ukaongezewa kiasi hicho. Pia tuangalie kwenye vyanzo vingine vya mapato kama wenzetu wengine walivyosema ili tu Mfuko wa Maji upate fedha. Kama walivyosema wenzangu na mimi nawaunga mkono kwamba maji ni kitu muhimu sana katika maisha ya binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu katika Mkoa wetu wa Iringa tumekuwa na matatizo makubwa sana, tumekuwa na vifo vingi sana vinavyosababishwa na ukosefu wa maji. Nitatoa mifano miwili ambayo imetugusa sana wananchi wa Iringa. Kwanza, kuna mwanamke ambaye alikuwa amejifungua watoto mapacha akaenda kwenye Mto Lukosi kwenda kuchota maji yule mama akauawa na mamba. Hili ni jambo ambalo kwa kweli linatuumiza, aliacha watoto wadogo sana.

La pili, juzi tu hata mwezi haujaisha, kuna mtoto wa shule ya sekondari ya Lukosi alikwenda pale kuchota maji akatokea mbakaji mmoja akamchukua yule mtoto kutaka akambakie upande wa pili. Watu walipotokeza akamtupa kwenye maji yule mtoto akafa. Kwa kweli ilitusikitisha sana kwa sababu yule binti alikuwa bado mdogo. Kwa hiyo, tunaomba sana Mkoa wa Iringa unauhitaji mkubwa sana wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika vituo vya afya vingi vilivyopo vijijini bado maji ni tatizo, inasababisha akina mama wakati wanajifungua wanapata mateso makubwa sana. Aidha, mama anaamka asubuhi kwenda kwenye shughuli ya kutafuta maji badala ya kwenda kwenye shughuli ya maendeleo. Hii pia inamkosesha mama kuendelea na miradi aliyonayo, kutwa nzima anatafuta maji, anamuacha pia hata mzee, hata ndoa nyumbani zinavunjika kwetu Iringa kwa sababu ya maji kwa sababu mama anaondoka saa
9.00 za usiku kwenda kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nisisahau kuwazungumzia wananchi wa Mji Mdogo wa Ilula. Bahati nzuri Mheshimiwa Rais alipokuja kuomba kura alikuja kwenye Wilaya ya Kilolo, lakini kwenye Mji Mdogo wa Ilula. Ule mji kama alivyosema Mheshimiwa Mgonokulima kwa kweli maji ni tatizo kubwa sana. Siku ile wananchi walikuwa wana mabango ynayozungumzia tatizo la maji wakimwambia Rais wanavyopata shida ya maji. Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba angeweza kuleta maji baada tu ya kuchaguliwa na akatuambia kwamba Waziri atakayemchangua atakuja mara moja kuja kusikiliza tatizo la maji. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri hebu aende Kilolo pale Ilula ukawaeleze kwa nini mpaka leo maji hayajaletwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mkoa wa Iringa hauna tatizo la maji bali ni usambazaji wa maji. Tunavyo vyanzo vingi sana vya mito kama Mto Ruaha, Mto Lukosi, Mto Mtitu na kadhalika, ni kwa nini Serikali isitumie mito hiyo kutatua tatizo hili la maji kwa sababu tumeona miradi mingi sana ya visima haifanyi kazi. Nilishauliza hata swali, tunayo mito mingi kama Mto Lukosi umezunguka maeneo mengi sana, lakini mpaka leo hii haujaweza kutumika ili uweze kuwasaidia wananchi wa Iringa kutatua tatizo la maji linalowakabili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba tu nipate majibu, katika mji huo huo wa Ilula, kulikuwa kuna wafadhili wa Austria. Je, ule mradi umefikia wapi kwa sababu tulijua kwamba ungeweza kuwasaidia wananchi wa pale Ilula?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja lakini nitaandika kwa maandishi kwa sababu mengi sana sijayazungumza. Nashukuru sana kwa kupata nafasi hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri Dkt. Tizeba, Naibu Waziri Mheshimiwa Olenasha, Watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea bajeti yao ili tuweze kuipitisha Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, napenda kuongelea kuhusu bima ya kilimo. Ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kuwapatia elimu wananchi ili waweze kuweka bima kwa ajili ya kilimo? Kwa sababu kilimo chetu nchini kimekuwa hali ya hewa haitabiriki na pia Serikali haijaweza kuwa na uwezo wa kutoa pesa ya kutosha kwa ajili ya miradi ya umwagiliaji. Tulipotembelea nchi ya China tulijifunza mengi yanayohusu kilimo mojawapo ni kuwaelimisha wananchi kuwa na Mashirika ya Bima ya Kilimo ili pia itawasaidia hata kukopesheka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Benki ya Kilimo. Tunaipongeza Serikali kwa kuanzisha Benki ya Kilimo nchini ambayo ilikuwa ndiyo kilio chetu na tukiamini ndiyo mkombozi kwa wakulima ambao ndiyo walio wengi. Ni kwa nini benki hii Makao Makuu yasiwekwe Dodoma ambako ndiyo katikati ya mikoa yote iwe rahisi na kuweza kufikika kirahisi? Vilevile ni kwa nini benki hii isiweze kufunguliwa madirisha katika mikoa na wilaya ili kuwatendea haki wakulima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kilimo cha umwagiliaji. Mkoa wa Iringa una eneo linaweza kumwagiliwa lenye jumla ya hekta 54,446, kati ya hekta hizo zinazomwagiliwa kwa sasa ni hekta 25,575 sawa na asilimia 47 ya eneo lote. Mazao makuu yanayolimwa kwa skimu za umwagiliaji ni pamoja na mpunga, mahindi, nyanya, vitunguu, mbogamboga na matunda. Mkoa wetu una jumla ya skimu za umwagiliaji 48 katika mchanganuo ufuatao; Iringa 32, Kilolo tisa (9), Mufindi tano (5) na Manispaa ya Iringa mbili (2).

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii miradi ya Manispaa ya Iringa ni miradi ya muda mrefu sana, Serikali imekuwa haitoi pesa kwa ajili ya miradi hii na tunategemea miradi hii ingeweza kusaidia vijana wetu hawa wa mjini waweze kujiajiri kupitia kilimo. Je, Serikali inatumia vigezo gani kutoa pesa kwa miradi hii ya kilimo cha umwagiliaji? Pia baadhi ya miradi ya umwagiliaji maji kutokamilika vyema na mingine haihitaji ukarabati wenye gharama kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za jumla katika kilimo katika Mkoa wetu wa Iringa ni kama zifuatazo:-

(a) Mtawanyiko mbaya wa mvua/ukame unaochangiwa na mabadiliko ya tabianchi;

(b) Uhaba wa mikopo yenye riba nafuu na isiyohitaji dhamana kubwa kwa kuwa wakulima wengi hukosa vitu vya kuwekea dhamana;

(c) Kuendelea kupungua kwa rutuba katika udongo suala linalosababisha wakulima wengi kuwa na mahitaji ya matumizi makubwa ya mbolea;

(d) Bei kubwa ya pembejeo za kilimo hasa mbolea na mbegu bora kunakosababisha wakulima gharama za uzalishaji wa mazao ya kilimo kuongezeka mara kwa mara;

(e) Magonjwa ya mimea hasa nyanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali inasaidiaje changamoto hizo kwa sababu asilimia 75 ya wananchi wa Iringa ni wakulima na ndiyo wanaochangia pato la mkoa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Joyce Ndalichako na Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha bajeti yao ili tuijadili. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kumteua Dkt. Ave Maria Semakafu kuwa Naibu Katibu Mkuu katika Wizara hii, hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuunga mkono hotuba ya Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na hasa ukurasa wa 29 wa kitabu chao. Serikali itoe tamko rasmi juu ya wanafunzi wa kike ambao wamekuwa wakifukuzwa shule kutokana na kupata ujauzito kurudishwa shuleni ili waendelee na masomo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu madeni ya walimu, niipongeze Serikali kwa kulipa madeni ya walimu kwa kuanza kulipa shilingi billion 33.1 sawa na asilimia mbili. Naiomba Serikali iongeze kasi ya ulipaji madeni hayo.

Katika Mkoa wa Iringa, walimu wanaidai Serikali shilingi 1,238,841,517.00, lakini tangu wamehakikiwa hakuna hata Wilaya moja iliyolipwa kabisa. Naomba kujua utaratibu unaotumika au vigezo vinavyotumika kulipa haya madeni katika mikoa na Wilaya zetu. Inakatisha tamaa sana kuona mwalimu anafundisha bila ari na chama kinataka kuandaa maandamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu bure, niipongeze Serikali kwa ujenzi wa mabweni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Niipongeze Serikali kwa programu hii, imeonesha kuwa kuna changamoto nyingi sana zilizojitokeza katika utekelezaji wa sera hiyo, lakini bila kuanza tusingezibaini changamoto hizo. Lakini ni vema Serikali iwe na mkakati wa kuzishughulikia changamoto kwa wakati ili azma ya Serikali iweze kutimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuta Kodi ya Ujuzi (SDL) na uchangiaji wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) katika vyuo vikuu binafsi, ukisoma ukurasa wa 33 katika kitabu cha Kamati, unazungumzia kwa kirefu kuhusu hilo, naomba niunge mkono hoja. Hivyo vyuo havifanyi biashara bali vinatoa huduma kwa manufaa ya nchi yetu. Kuwepo kwa tozo hizi kunapelekea kuwa na changamoto ya kupanda kwa ada na kupungua kwa ajira ili vyuo viweze kujiendesha, Serikali iliangalie upya jambo hili na kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za elimu zilizopo katika vyuo vyetu vya Iringa, bei za nyumba katika maeneo yanayozunguka vyuo vya Iringa ni kubwa mno, ni vema Serikali ingetoa bei elekezi. Mikopo bado inachelewa sana, hasa wanafunzi wa elimu ya vitendo (field and research).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundombinu ya watu wenye ulemavu, niipongeze Serikali kwa kusambaza vifaa vya kujifunzia na kufundishia lakini bado miundombinu katika shule nyingi si rafiki na watu wenye ulemavu kabisa. Mazingira ya vyoo vya shule nyingi bado si rafiki kwa watoto wa kike hasa wawapo kwenye siku zao. Uwiano uliopo kati ya idadi ya wanafunzi na idadi ya matundu ya vyoo bado si ya kuridhisha kwa viwango vya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hali mbaya sana ya majengo ya shule; hali ya majengo ni mbaya sana, mfano katika Mkoa wetu wa Iringa shule nyingi tangu zijengwe hazijawahi kukarabatiwa, sera ipo vipi? Mtoto anasoma katika mazingira magumu sana, hakuna vioo, hakuna floor, hakuna ceiling board.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maktaba katika shule zetu, sera inasemaje kuhusiana na hili? Hali ya maktaba za shule za msingi na sekondari si nzuri, watoa huduma za maktaba (wakutubi) hawapati ajira kwenye maktaba za shule. Shule inapohamishwa inatakiwa iwe na maktaba lakini si shule zote zenye maktaba. Kama tusipozisimamia hizi maktaba hatutakuwa tumemtendea haki huyu mtoto tunayetaka kumjenga kielimu na kuwa na mazoea ya kujisomea ambayo ingemsaidia hata akienda elimu ya juu kuwa na utaratibu wa kusoma.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie changamoto zilizopo katika Mkoa wetu wa Iringa kama ifuatavyo:-

(i) Ukosefu wa fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati mkubwa kwa baadhi ya miradi kama Tanangozi, Kidabaga, Malangali na Mbalamaziwa;

(ii) Ukosefu wa fedha kwa ajili ya ujenzi wa miradi mipya vijijini kama Mkonge – Igoda, Ukelemi na Uyela – Nyololo, Njiapanda na Makungu;

(iii) Uwezo mdogo wa wakandarasi na wataalam washauri kifedha na kitaalam katika kujenga na kusimamia mradi wa maji;

(iv) Ukosefu wa elimu ya kutosha kwa wananchi juu ya uchangiaji wa huduma ya maji na uendeshaji wa miradi ya maji vijijini; na

(v) Upungufu wa wataalam wenye sifa katika Halmashauri za Wilaya na Mamlaka za Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya LAAC
ilipotembelea katika Mkoa wetu wa Iringa ilibaini yafuatayo:-

(i) Miradi mingi ilikosewa wakati wa usanifu, hivyo, visima vingi kwa sasa havina maji na kama yapo basi sio ya kutosha;

(ii) Miradi mingine chanzo cha maji kimehama na hivyo kukosa maji katika chanzo;

(iii) Baadhi ya wakandarasi hawana uwezo wa kifedha na kusababisha miradi kutokamilika kwa wakati; na

(iv) Ucheleweshwaji wa wakandarasi kupatiwa malipo wanapowasilisha certificates mpaka kupelekwa mahakamani kwa baadhi ya miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua tatizo linalosababisha Serikali kutotumia mito mingi tuliyonayo katika mkoa wetu kama Mto Ruaha, Mto Lukosi, Mto Mtitu katika kutatua tatizo kubwa la maji badala ya miradi ya visima inayotumia pesa nyingi na hakuna maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya umwagiliaji. Katika Mkoa wetu wa Iringa na hasa Jimbo la Iringa, ipo miradi miwili ya umwagiliaji ya Ruaha Irrigation Scheme, huu upo Kata ya Ruaha na Mkoga Irrigation Scheme, huu upo katika Kata ya Isakalilo. Miradi hii ni ya siku nyingi sana, Serikali haijaweza kuitengea pesa ili iweze kukamilika na kutoa ajira kwa wananchi. Nataka kujua vigezo vinavyotumika kupeleka hizi pesa za miradi ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, uvunaji wa maji. Ni lini Serikali itatoa elimu katika suala hili ili Halmashauri zetu ziweke utaratibu wa kuhakikisha maji yanavunwa wakati wa mvua nyingi ili kuwa na akiba ya maji wakati wa kiangazi? Hayo maji yangeweza kusaidia katika shughuli za kibinadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bustani za mboga (vinyungu). Mkoa wetu wa Iringa ni mkoa ambao wananchi wake wanafanya shughuli za kibiashara hasa za mbogamboga kutumia maeneo hayo nyevunyevu kujipatia kipato lakini Serikali imepiga marufuku. Sasa nini mpango
wa kuwasaidia hawa wananchi waliokuwa wanategemea kilimo hicho?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na Waislam wote nchini kwa kuwatakia mfungo mwema katika mwezi huu Mtukufu. Naomba mchango wangu nimtangulize Mwenyezi Mungu. Nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu wote wa Wizara pamoja na Watendaji wa Wizara kwa kutuletea hii bajeti ili tuweze kuijadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Benki ya Wanawake. Tanzania ina mabenki mengi lakini Benki ya Wanawake ni benki pekee ambayo ina wateja karibu asilimia 74 ya wateja wote. Sisi wanawake tunao wajibu mkubwa kabisa wa kuipigania benki hii. Mwaka 2010 Serikali ilitoa ahadi ya kutoa ruzuku ya shilingi bilioni 10 kwa miaka mitano yaani itatoa bilioni mbili kila mwaka katika Benki ya Wanawake lakini toka ahadi hiyo ilipotolewa ni shilingi bilioni 5.75 tu ambayo imetolewa mpaka sasa hivi. Je, hizi bilioni 4.25 Serikali itatoa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa sababu benki hii tumeona inakuwa ikifanya kazi vizuri sana, karibu mikoa sita sasa hivi imefungua madirisha lakini bado ina kazi kubwa kuhakikisha kwamba benki hii inafungua madirisha katika mikoa yote ili wanawake wote waweze kupata haki ya kupata mitaji kama ambavyo Serikali ilitaka, kwamba wanawake waweze kupata mitaji kupitia benki hii ya wanawake. Sasa nitaomba labda wakati Waziri anahitimisha atueleze na asipoeleza vizuri itabidi tushike shilingi ya mshahara wake ili wanawake wote nchini waone kwamba benki hii inatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kuzungumzia kuhusu TIB (Tanzania Investment Bank), naungana mkono na wote waliosema kwamba upo umuhimu wa benki hii kupewa mtaji wa kutosha kwa sababu ndio benki pekee inayosaidia kuleta kwa haraka zaidi maendeleo ya nchi hii. Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa viwanda lakini bila kuiwezesha benki hii tutapata shida sana, kwa sababu ndio pekee itakayosaidia kuwezesha miundombinu ya viwanda. Serikali iliahidi kuipatia mtaji shilingi bilioni 500 na tena iliahidi kutoa trilioni tatu lakini ilipatiwa shilingi bilioni 150 tu. Sasa niombe Serikali itakapokuwa inajibu itueleze nini mkakati wa kuhakikisha benki hii sasa inawezeshwa ili huu uchumi wa viwanda uweze kwenda kwa kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Naipongeza sana mifuko hii kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikifanya katika jamii yetu kama ujenzi wa daraja la Kigamboni, ujenzi wa majengo ya UDOM na kadhalika. Niiombe Serikali ilipe madeni ya mifuko hii ili iweze kuendelea kuisaidia jamii na Serikali pia. Kipekee naomba nichukue nafasi hii kuishukuru LAPF, NSSF, PPF na Shirika la Bima (NIC) kwa kuniunga mkono katika programu yangu ya ukarabati wa majengo kongwe kwa shule za msingi katika Mkoa wa Iringa. Niombe na mifuko mingine basi iendelee kutusaidia ili kuendelea kusaidia jamii zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alisema mifuko hii sasa hivi ianze kuwekeza katika viwanda ili isaidie pia na kuongeza ajira nchini. Pia nimshukuru Mheshimiwa Jenista Mhagama alipokuja Iringa kutembelea kinu cha National Milling alisema kwamba NSSF itatoa mtaji. Najua kwamba ikitoa mtaji katika kile kinu itasaidia pamoja pia na kupata soko kwa wakulima wetu wa Iringa vilevile kuongeza ajira katika mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuzungumzia kuhusu madeni ya wazabuni. Naipongeza Serikali kwa kuanza kulipa madeni ya wazabuni kiasi cha shilingi bilioni 796 kati ya deni la shilingi trilioni tatu iliyokuwa inadaiwa, lakini bado wazabuni wengi sana wakimemo wa Mkoa wa Iringa wanaidai Serikali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali ingetangaza katika gazeti ili wazabuni waliohakikiwa na wale waliolipwa madeni waweze kujua, kwa sababu kuna wengi walikuwa wanaidai, lakini hawajui hatma ya madeni yao mpaka leo hii, kama yatawekwa wazi angalau hata sisi tunapokwenda kwenye mikutano maswali yanapungua, wanakuwa wanajua kabisa hatma ya madeni yao ni yapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee kuhusu Ofisi ya Ukaguzi (CAG), kwanza niipongeze kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikiifanya, ofisi hii inafanya kazi nzuri sana lakini changamoto kubwa ni utekelezaji wa ushauri wa mapendekezo yanayotolewa katika ripoti yake. Bado Serikali hawajaweza kuyafanyia kazi yale mapendekezo ambayo yanatolewa. Vilevile wapewe fedha ya kutosha, kwa wakati na waweze kukagua mapema ili kusaidia nchi yetu panapokuwa na matatizo, tuweze kujirekebisha halafu tuendelee mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu TRA; TRA imekuwa ikifanya kazi nzuri sana tu lakini nafikiri sasa hivi wafanyabiashara wale wadogo wadogo wamekuwa wakikadiriwa kodi kubwa sana hata wale wakubwa kiasi kwamba wanashindwa kufanya biashara zao vizuri. Vilevile kuna utaratibu wa kumkadiria kodi mtu anayetaka TIN ya biashara, anatakiwa alipe kadirio hilo kabla hata ya kuanza biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limekuwa ni tatizo sana, watu wengi wanakwepa kuomba TIN kwa sababu wanakuwa wana mitaji midogo, sasa akijua kwamba akienda pale atatakiwa akadiriwe ile kodi yake kabla hata hajaanza biashara halafu baadaye tena ndio alipie anashindwa kujisajili. Sasa ningeomba Serikali iangalie kwa sababu shida yao ni kurasimisha hizi biashara ili kuweza kupata kodi kwa urahisi zaidi, lakini sasa hii itasababisha biashara nyingi kutorasimishwa, watu wanaogopa kwenda kuzirasimisha kwa sababu wanatakiwa walipe kodi hata biashara zao hawajui kwamba watazifanyaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna utaratibu wa kumtaka mfanyabiashara aambatanishe invoice ya madai kwa mtu aliyempatia huduma kabla hata yeye hajalipwa. Ukitolea tu mfano wale wazabuni wanaofanya kazi na Serikali utakuta kwamba wanapeka invoice lakini kuja kulipwa madeni inachukua muda mrefu sana. Sasa TRA wanataka uambatanishe na ile invoice ya risiti wakati hata bado hujalipwa. Hili pia ningeomba Serikali iliangalie na iweke utaratibu mzuri wa kumsaidia huyu mfanyabiashara ili aweze kufanya biashara yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lingine, utaratibu wa kutaka wafanyabiashara kununua hizi EFDs, nafikiri wenzangu wengi sana wamesema. Mfanyabiashara anakuwa na mtaji kidogo sana, sasa anapokwenda kununua hii EFD tayari mtaji wake unakuwa umeathirika. Kwa hiyo, hata hii niungane na wenzangu kwamba Serikali hebu iangalie uwezekano wa EFDs mashine ziweze kutolewa bure. Nakumbuka hata Mheshimiwa Rais alishawahi kutoa ushauri kwamba TRA wawapatie hizi EFDs mashine wafanyabiashara wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuchukulie tu mfano kama TANESCO utakuta TANESCO wanakufungia ile mashine yao kwa hiyo inasaidia, inapunguza hata gharama za kufuatilia. Hii ni kwa sababu tayari mtu anakuwa amefunga ile mashine na hata ile kodi inayokadiriwa sasa inasaidia, kwamba unalipa kweli kodi halali, lakini si kama wanavyokadiria kodi kubwa wakati pato unalopata sio. Kwa hiyo, naomba hizi EFDs ziweze kupatiwa bure kwa wafanyabiashara wote, hata Mkoa wa Iringa bado hatujapatiwa hizi mashine za EFDs. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna lile la tax clearance kwa mfanyabiashara anayedaiwa kodi. Naona kama sio sahihi kwa sababu utakuta mfanyabiashara huyu, wengi sana wamefunga biashara zao sasa hivi kwa sababu ya hizi tax clearance. Hii ni kwa sababu wamekadiriwa kodi kubwa ambayo kwa kweli hailipiki na hawa wafanyabiashara wamekuwa wakifanya biashara bila kupata faida. Utakuta huyu mkadiriaji bado hajaangalia na bado hajamsikiliza huyu mfanyabiashara matatizo makubwa ya kibiashara anayoyapata. Sasa hivi wengi wamekopa benki na utakuta wengi wao bado wanaidai Serikali na wengi wao bado wana matatizo makubwa kwenye biashara zao. Kwa hiyo, ningeomba Serikali iangalie sana hawa wafanyabiashara kwa sababu ni sawasawa na ng’ombe… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria muda wa mzungumzaji kuisha)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa uwasilishaji wa bajeti yao hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali ikifanya juhudi za kurasimisha biashara zisizo rasmi, Wizara ya Fedha kupitia TRA haioneshi juhudi za makusudi kuwakomboa wananchi wa hali ya chini kuinuka kiuchumi na kuweza kuchangia pato la Taifa kutokana na taratibu ngumu zilizowekwa kwa wafanyabiashara katika kuanzisha na kuendesha biashara zao. Taratibu hizo ni pamoja na:-

(i) Kumkadiria kodi mtu anayetaka TIN ya biashara na anatakiwa alipe kadirio hilo kabla ya biashara kuanza;

(ii) Kumtaka mfanyabiashara aambatanishe invoice yake ya EFD receipt wakati wa kuwasilisha invoice ya mradi kwa mtu aliyempatia huduma kabla hata yeye hajalipwa, mfano Idara za Serikali ambapo malipo yenyewe hayalipwi kwa wakati;

(iii) Kuwataka wafanyabiashara kununua EFD machine kwa fedha zao chache za mtaji wakati EFD ni machine inayoiwezesha TRA kukusanya mapato yake. Ni kwa nini tusifanye kama TANESCO ambapo mita ya umeme inakuwa mali ya TANESCO hivyo kuipunguzia gharama ya ufuatiliaji wa madeni ya kodi? Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Tano alitoa na kuzigawa bure ili zisaidie kukusanya kodi lakini utaratibu huo ulifanyika kwa kipindi kidogo tu na haukuendelea tena;

(iv) Kuzuia ugawaji wa Tax-Clearance kwa mfanyabiashara anayedaiwa kodi jambo ambalo si sahihi kwani kunamkwamisha mfanyabiashara huyo kuendelea kufanya biashara ili aweze kupata fedha ya kulipia deni la kodi anayodaiwa ukitilia maanani kuwa hata leseni haitolewi kwa mtu asiyekuwa na Tax Clearance. Kwa nini usiwepo utaratibu mwingine wa kumruhusu huyu mtu akaendelea kufanya biashara wakati mwingine anakuwa anakadiriwa makadirio ya kodi makubwa kuliko pato halisi. Akinyimwa Tax Clearance anashindwa kuomba kazi matokeo yake anafunga biashara. Serikali inawavunja moyo wasifanye biashara halali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuanza kulipa madeni ya wazabuni kiasi cha shilingi bilioni
796.22 kati ya kiasi cha shilingi trilioni tatu kinachodaiwa. Hata hivyo, bado wazabuni wengi wanadai labda ni vizuri Serikali itangaze katika magazeti wazabuni waliohakikiwa na wale waliolipwa madeni ili waweze kujua sababu kuna wengine walikuwa wanadai lakini hawajui hatima yao mpaka leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Wanawake ilianzishwa ili kuweza kuwasaidia wanawake kupata mtaji wa biashara baada ya kuona udhalilishaji mkubwa wanaopata katika baadhi ya taasisi. Mwaka 2010 Serikali ilitoa ahadi ya kuipatia Benki ya Wanawake shilingi bilioni 10 kwa miaka mitano maana yake shilingi bilioni mbili kila mwaka. Mwaka 201/2012 – Serikali ilitoa shilingi bilioni mbili; 2012/2013 – Serikali ilitoa shilingi bilioni 1.75 na 2013/2014 – Serikali ilitoa shilingi bilioni 1.5. Jumla Serikali imeweza kutoa shilingi bilioni 5.75. Je, shilingi bilioni 4.25 itatolewa lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, TIB (Tanzania Investment Bank), Tanzania tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda lakini bila kuiwezesha benki hii tutapata shida sana, sababu ndiyo benki itakayosaidia kuwezesha miundombinu ya viwanda. Serikali iliahidi kuipatia mtaji wa shilingi bilioni 500 na tena shilingi trilioni tatu lakini walipatiwa shilingi bilioni 150 tu. Je, nini mkakati wa kuisaidia benki hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na pongezi kwa Waziri wetu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya kwa ajili ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mkoa wa Iringa ina eneo finyu sana kutokana na muingiliano wa Gereza Kuu la Iringa na kusababisha Madaktari wetu Bingwa kuishi nje ya hospitali. Tunaomba kwa sababu Serikali ni moja, Gereza liondoke kupisha hospitali ili hata kuweza kujenga majengo mengine ya huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Iringa una upungufu wa wafanyakazi asilimia 60. Changamoto hii inasababisha matatizo makubwa sana mpaka katika Hospitali za Wilaya. Pia tuna changamoto Hospitali ya Mkoa haina Daktari Bingwa wa Watoto. Tunaomba Serikali iangalie kwa uzito mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu dawa MSD; niipongeze Serikali kwa upatikanaji wa dawa na nipongeze kwa kuleta moja kwa moja katika vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Bima ya Afya, tunaiomba Serikali suala la wazee, huduma ya wazee dawa ni ghali sana zipo nje ya mfumo wa bima yao, wanapata shida sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie watoto yatima walio katika vituo wanapata shida sana hawana bima ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango gani wa kuweka madawati katika vyuo vikuu. Nilipata bahati ya kukutana na Serikali za Wanafunzi wa Vyuo Vikuu. Wanafunzi wanachangia pesa lakini haziwasilishwi Bima ya Afya kwa wakati kwa ajili ya kupatiwa kadi za matibabu. Naomba Wizara ilichukue hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu tatizo la ugonjwa wa saratani; niipongeza Serikali kwa kuanza kutoa chanjo kwa mabinti zetu kuanzia miaka tisa hadi 15; hii ni hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupata ufafanuzi je, watoto wa kiume hawana haja ya chanjo hii? Huwa naona kuna kansa ya mabusha. Je, inawezekana chanjo hii wakapatiwa wanawake wenye umri wa zaidi ya miaka 15? Nimeona nchi nyingine wanapatiwa. Ni imani hata mkiweka malipo kwa ajili hiyo au bima ziweze kulipia chanjo hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo tatizo kubwa sana kwa wagonjwa wa saratani katika Mkoa wa Iringa kwenda Hospitali ya Ocean Road Dar es Salaam ni kwa nini Serikali isiweke centre za haya matibabu kikanda au matibabu yasogezwe Dodoma ili iwe rahisi kufikiwa na kupunguza gharama kwa sababu kina mama wanapata shida sana hata kimaisha wapokwenda Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu huduma ya matibabu ya moyo na figo; pongezi kubwa sana huduma hiyo imetupa moyo sana kuwa imeweza kupunguza hata gharama za matibabu ya nje ya nchi. Hongera sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kuwapongeza, Waziri Mheshimiwa Lukuvi, Naibu Waziri Mheshimiwa Angelina Mabula, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kuleta bajeti hapa Bungeni ili tuijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Migogoro ya Ardhi, niipongeze Wizara na Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii kwa kuendelea kutatua migogoro mingi nchini ikiwemo ya wakulima na wafugaji. Ni kwa nini Serikali isingetenge maeneo ya wafugaji peke yake na yakaainishwa na yakawekewa miundombinu kwa ajili ya kuwezesha wafugaji kutohama hama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ipo migogoro inayowahusu Maafisa Ardhi katika Halmashauri zetu. Tunashukuru hata hivi Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wanafanya juhudi kubwa sana kuwasaidia wanyonge waliokuwa wakipokonywa ardhi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanagawiwa ardhi ya eneo moja zaidi ya watu wawili na kusababisha usumbufu mkubwa sana, lakini huwa tunapata tabu sana, Afisa anayeharibu Halmashauri moja badala ya kubadilisha anahamishiwa eneo lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa Wataalam wa Ardhi; Halmashauri zetu nyingi nchini bado zina upungufu mkubwa na kunasababisha wananchi wengi kupata usumbufu mkubwa wanapotaka kupimiwa ardhi au kupata hati na sasa hivi na hili la vyeti feki nalo limechangia kwa kiasi kikubwa sana kuendelea kuwa na idadi ndogo ya wafanyakazi. Ni vizuri Serikali ikaweka utaratibu wa kujua nafasi hizi mapema ili kusaidia utendaji katika Halmashauri zetu na kupunguza kero kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mipango Miji, ni kwa nini miji yetu mingi haijapangwa, je kazi ya Maafisa Mipango Miji ni nini? Kumekuwa na mwingiliano mkubwa sana wa shughuli katika miji yetu kama vile hakuna wataalam. Ushauri wangu ni vizuri Maafisa Mipango Miji wangekuwa wanasimamia ile michoro iliyopangwa au kama miji haujapangwa basi wasigawe viwanja kabla ya kupitishwa michoro. Hata hivyo, kuna maeneo ambayo hayajapimwa ungekuwepo utaratibu maalum ili kuweza kusaidia jamii, kwa sababu kuna baadhi ya maeneo hayafikiwi kihuduma, wananchi wamekuwa wakipata mateso makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu NHC, niipongeze Serikali kwa ajili ya kazi nzuri inayofanywa na Shirika hili, lakini tuombe majengo haya yajengwe hata katika miji midogo sababu hata wafanyakazi wanapata shida sana wanapohamishiwa mikoani. Ni kwa nini Halmashauri zetu zisitenge maeneo na kuingia ubia nao ili iweze kusaidia upungufu uliopo katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, haya mashirika yanayojenga nyumba kwa ajili ya Walimu kama Watumishi Housing nao wangefika katika Halmashauri zilizopo pembezoni ambako kuna matatizo makubwa sana ya nyumba za watumishi wakiwemo Walimu hata kama ya
kawaida sana ya vyumba vitatu au viwili ili kuyafanya maeneo hayo pia wafanyakazi waweze kuishi kama mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malalamiko ya ukarabati wa nyumba za mjini, naomba kujua je kuna sheria yoyote iliyotolewa na Serikali nyumba za kati kati ya mji zisikarabatiwe zijengwe maghorofa. Sababu kunakuwa na malalamiko kwa wananchi wa Manispaa ya Iringa kutopatiwa vibali vya kukarabati nyumba zao hata kama ni magofu na kusababisha majengo mengi kuwa na hali mbaya sana. Sababu hawana uwezo wa kujenga maghorofa sasa tunaomba Serikali itupatie ushauri. Sasa hivi hakuna wawekezaji kabisa kutokana na hali ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuipongeza Serikali kwa kazi wanayoifanya. Nilichangia kwa kuongea, sasa nataka kuongeza mchango wangu kwa maandishi. Niendelee kumpongeza Mkurugenzi wa TTCL, Mwenyekiti wa Bodi na watendaji wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba Serikali ilipe madeni ya TTCL kwa sababu kuna Mashirika ya Umma na Taasisi za Serikali ambazo zina madeni makubwa na ya muda mrefu sana ili kampuni iweze kujiendesha kiushindani na Vodacom, Tigo, Airtel na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilikuja na mpango mkakati wa kuboresha Shirika la Posta. Je, mkakati huo umeishia wapi? Majengo yao yanahitaji ukarabati, vifaa vya kisasa vya kazi, pamoja na maslahi ya wafanyakazi. Nina imani kama Serikali itafanya maboresho, shirika hili litajiendesha kwa faida kwa sababu lilikuwa na mali za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa Posta Kodi na Anwani za Makazi ni muhimu sana kwa Taifa letu, utasaidia uchumi wa nchi, utarahisisha kupeleka mizigo na utasaidia hata TRA kukusanya kodi za majengo. Mbaya zaidi mwaka 2016/2017 Serikali ilitenga shilingi bilioni tatu; zilizotolewa ni shilingi milioni 95 tu sawa na asilimia tatu; mwaka 2017/2018 zilitengwa shilingi bilioni tatu lakini Serikali haikutoa pesa yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali italeta sheria, kwani miundombinu katika vyombo vya usafiri inakuwa siyo rafiki kabisa na watu wenye ulemavu hawawezi kutoka point A kwenda point B, kwa sababu baiskeli yake haiwezi kupakia katika chombo cha usafiri. Bado hata baadhi ya majengo siyo rafiki kabisa kwa watu wenye ulemavu. Mfano, majengo ya huduma ya hospitali, vituo vya afya, mashule hata hili Jengo tu la Bunge pamoja na kufanyiwa ukarabati bado Wabunge wenye ulemavu hawawezi kuyafikia majengo yaliyopo katika maghorofa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali yetu, lakini ni vema sasa deni la makandarasi na wahandisi washauri wa miradi ya barabara wakalipwa pesa yao ya shilingi bilioni 711.13.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitengo cha TEMESA ni muhimu sana hasa Kitengo cha Ufundi (karakana). Ni kwa nini Serikali isiweke mkakati wa kuwa na vitendea kazi na ukarabati katika karakana za mikoa ili kitengo hiki kiweze kusaidia matengenezo ya magari yote ya Mashirika ya Umma na Taasisi za Serikali na iweke bei ambazo zingeweza kuvutia hata taasisi za watu binafsi ili waweze kutumia karakana hizo na kuweza kujiendesha kifaida kuliko ilivyo sasa kwamba karakana hizi huduma zake zimekuwa na bei kubwa sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali kwa kuwashirikisha wanawake katika kazi za barabara kwa makandarasi wanawake. Ushauri wangu ni kwamba ni vema ushirikishwaji huo ungewekewa utaratibu wa kila Ofisi za TANROADS Mkoa kuendesha hayo mafunzo ya kuwajenga uwezo wanawake ili wanawake wote wapate fursa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nianze na dua la kukuombea, naomba Mwenyezi Mungu akujalie, akupe afya njema na wote wanaokutakia mabaya washindwe kwa Jina la Yesu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na pongezi kubwa kabisa za kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwasilisha hotuba yake; na nimpongeze Mheshimiwa Jenista, Mheshimiwa Mavunde na Mheshimiwa Ikupa.

Mheshimiwa Spika, pia niwaambie wenzetu mwenye macho haambiwi ona, hivi kazi zote ambazo Mheshimiwa Rais, ambazo Serikali hii imezifanya, miradi mingi imefunguliwa, kila siku Mheshimiwa Waziri Mkuu anakwenda huku na huku, kweli hamuioni jamani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe tu niseme kwamba, ukisoma ukurasa wa 10 unaonesha kabisa wananchi wameanza kuelewa sera za Chama cha Mapinduzi, wamehama wengi sana. Katika uchaguzi tu kati ya 59; 58 tumeshinda CCM na Wabunge wote majimbo yote tumeshinda na niwapongeze hata Wabunge ambao wamehama upande ule wakaja upande huu wa kwetu; hongereni sana kwa kuja huku wala hamjakosea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, niwapongeze Mawaziri wote waliopo katika Serikali hii bila kuwasahau wanawake wenzetu; hamjatuangusha wanawake, mmefanya kazi vizuri sana tu. Kila siku tunawaona mnahangaika huko na huko kwa kweli mko vizuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na kuchangia kuhusu uwezeshaji kwa vijana. Niendelee tu kuipongeza Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi kwamba, walikuja Iringa wakafungua yale mafunzo ya vijana katika Chuo cha Don Bosco, Mheshimiwa Jenista nakushukuru sana. Vijana wengi sana wameitikia mwitikio mkubwa sana katika kile chuo mpaka kumetokea changamoto kubwa vijana wengi wanakosa sehemu za kusoma kwa sababu zile nafasi ni chache. Tungetamani hata kila wilaya yale mafunzo yaendeshwe ili vijana wengi waweze kupata yale mafunzo. Pia, kuna changamoto kwamba, vijana wale miezi sita sasa hawajapata posho, labda hilo liangaliwe ili waweze kupata wasisome kwa shida sana.

Mheshimiwa Spika, vile vile tulikuwa tunaomba pengine iwepo connection kati ya wakuu wa wilaya pamoja na chuo ili kuratibu maana imekuwa malalamiko yanatufuata sisi Wabunge tunashindwa sasa twende wapi. Tunaomba pia, hilo liangaliwe. Pia, uwepo utaratibu mzuri kuhakikisha kwamba, wale wanaohitimu yale mafunzo angalau pia halmashauri zao ziweze kuwapatia asilimia tano ile ya mikopo. Pia kama kuna kazi basi wapewe za kutengeneza madawati, chaki na kadhalika ili ile mikopo iwe rahisi kuweza kurejeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Jenista, niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Mavunde wamefanya kazi nzuri sana kufuatilia mikataba ya wafanyakazi katika viwanda, katika makampuni yale ya wawekezaji. Sasa niombe, sasa hivi waelekee kwenye hizi sekta ambazo si rasmi; kwa mfano wafanyakazi wa ndani wanafanya kazi kwenye mazingira ambayo bado ni magumu sana.

Mheshimiwa Spika, najua wengine waajiri wao mko humu ndani, lakini mtanisamehe lazima niwasemee, wengi wametoka kwenye Mkoa wetu wa Iringa, bado malalamiko yao ni makubwa sana hawatendewi haki. Vile vile kuna wafanyakazi ambao wanafanya kazi kwenye migahawa nao bado mikataba yao si mizuri. Hawa wenzetu wanaofanya kazi kwenye baa nao wanafanya kazi kwenye mazingira magumu ingawa ile bia yenyewe inatuletea faida kubwa sana katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nisisahau kabisa naomba niwasemee wenzetu waandishi wa habari, wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana tunaonekana kwenye TV, wanatuandika kwenye magazeti, lakini nao pia mikataba yao si mizuri sana kwa sababu utakuta bado wengine hawana hata bima hizi za afya, hawana bima za maisha, wanahatarisha hata maisha yao. Vile vile tunatakiwa tuwasaidie ili wafanye kazi kwenye mazingira mazuri waendelee kujenga Taifa letu kwa kuandika vizuri. Mishahara yao pia, bado haieleweki, kila mwajiri anamwekea vyovyote anavyotaka; kwa hiyo, niombe kabisa pia, waangaliwe.

Mheshimiwa Spika, niendelee katika sekta ya afya. Niendelee kuipongeza Serikali kwa sababu, wamepunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa kwenye hospitali na vituo vya afya, lakini kuna changamoto kwenye Hospitali yetu ya Mkoa wa Iringa. Kwamba eneo lile ni dogo sana na lina mwingiliano na magereza. Tulishawahi kusema na Waziri wa Mambo ya Ndani analijua na Naibu Waziri wa Afya naye si muda mrefu alikuwa kule ameona.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo inasababisha Madaktari wetu Bingwa wanakaa nje ya hospitali, kwa hiyo inakuwa shida sana kuwahudumia wagonjwa wanapopata shida usiku. Vile vile tuna changamoto ya Daktari Bingwa wa Watoto, hakuna kabisa kwenye hospitali yetu ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, vile vile upungufu mkubwa sana wa wafanyakazi sekta ya afya, karibu asilimia 60 ni tatizo katika mkoa mzima; na Hospitali ya Wilaya ya Mufindi yenyewe inaongoza kwa sababu asilmia 40 hakuna wafanyakazi. Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie kuziba zile nyufa za wafanyakazi ambao waliondolewa ili wagonjwa waweze kutendewa haki.

Mheshimiwa Spika, niipongeze pia Serikali kwa mgawo wa 4.5 billion katika wilaya zetu kujenga hospitali za wilaya katika mkoa wetu; Wilaya ya Kilolo, Wilaya ya Mufindi, Iringa DC. Japokuwa katika hospitali ya manispaa hatujatengewa kitu chochote na kuna changamoto kubwa ya jengo la vipimo hakuna kabisa na kuna mashine za X-Ray, CT-Scan, Ultrasound, hakuna kabisa. Vilevile wodi za kulaza wagonjwa wengine pia, hakuna na tulikuwa tunategemea kwamba, ile hospitali ingepunguza msongamano wa wagonjwa wa hospitali ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, najua kwamba, Mheshimiwa jafo alishapita na kuona hizi changamoto, kwa hiyo niombe kwa kweli zifanyiwe kazi. Mashine hizi zitakazopatikana zitasaidia hata gharama ndogondogo za kuiendesha ile hospitali. Vile vile huduma ya wazee dawa ni ghali sana, zipo nje ya mfumo, kwa hiyo huduma zile ambazo ziko nje ya mfumo wa bima yao wanapata shida kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kukaa na wafanyabiashara na kusikiliza changamoto zao. Ni kweli tozo katika viwanda zimekuwa nyingi sana, ningeomba kwa kweli waziangalie ili tuendelee kuhamasika na huu uchumi wa viwanda, ili viwanda vingi viweze kufunguliwa.

Mheshimiwa Spika, nichukulie tu mfano mdogo kwenye sekta ya maziwa. Unaona TFDA ile yogurt wana- charge flavor dola 3,000, lakini hii ingechajiwa tu labda kwa zao lenyewe la maziwa bila kuangalia kila flavour kwa sababu mtu akiwa na flavour 10 anachajiwa (charge) dola 3,000. Kwa hiyo, naona hii pia, Waziri wa Mifugo aliangalie.

Mheshimiwa Spika, vilevile OSHA. Hii OSHA wanapima afya za wafanyakazi unalipia Sh.80,000, Manispaa nao wanapima afya za wafanyakazi wanalipia tena; sasa hii ingewekwa kwenye sekta moja, ili zote zichajiwe (charge) kwa pamoja. Hii inawakatisha sana watu wanaofanya kazi katika sekta hii ya maziwa.

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi kuna watendaji wengine hawaitakii mema hii nchi yetu, kwa sababu kwa mfano tarehe tatu mwezi wa nne walikamata gari la maziwa la ASAS pale Iringa. Lile gari lilivyokamatwa limekamatwa kuanzia saa 12.00 limekuja kuachiwa saa 6.00 wamechajiwa (charge) 1,000,000/= kwa kosa ambalo kwa kweli, ukilisikiliza wala si kosa.

Mheshimiwa Spika, sasa hapohapo ukatokea uharibifu wa packets 3,000 takriban 3,500,000/=. Sasa hii inaleta matatizo sana kwa wenzetu ambao tunatagemea kwamba, wangetusaidia hata uajiri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja hii, kwa yale ambayo sijachangia nitachangia kwenye Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya na kwa kweli wanaombeza labda hao ni wanga tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa pamoja na Naibu wake wote kwa kazi nzuri ambazo wamekuwa wakizifanya katika Wizara hii. Wamezindua miradi mingi sana ukiwepo ununuzi wa ndege na ujenzi wa reli ya umeme, niwapongeze sana. Kutokana na kazi nzuri ambayo reli imekuwa ikifanya kuna ule mfuko wake pengine wangeachiwa maana unachukua muda mrefu na wao wana kazi nyingi na tunajua kwamba tunataka reli hii ikamilike mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niipongeze Serikali kwa ujenzi wa kiwanja cha ndege, mwenzangu amepongeza na mimi napongeza. Kupitia World Bank Kiwanja chetu cha Nduli kitajengwa ikiwa package mojawapo na ile barabara inayokwenda mbuga za wanyama. Kwa kweli naamini kabisa Mkoa wetu wa Iringa sasa tutapata uchumi wa kutosha na utafunguka kiutalii kwa sababu tukishajenga uwanja na tukishapeleka barabara ya lami Ruaha National Park najua kwamba Nyanda za Juu Kusini na Mkoa wa Iringa pia utafunguka kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee kupongeza Serikali kuhusiana na ujenzi wa mtandao wa barabara nchini ikiwepo barabara ya Dodoma - Mtera - Iringa kilometa 260. Kwa kweli barabara hii imekuwa mkombozi sana kwetu, inatufanya dakika dakika mbili tumefika Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ipo changamoto kubwa pale, ningeomba Mheshimiwa Waziri aangalie na ikiwezekana labda twende akaiangalie vizuri zaidi pamoja na wataalam wake. Wakati wa mvua ile barabara mawe yanadondoka kiasi kwamba kuna wakati magari hayapiti kabisa. Kwa hiyo, tumemwona hata Meneja wa TANROARDS, Ndugu Kindole, karibu siku tatu amefanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo, naomba kabisa barabara hiyo iangaliwe kwa sababu kuna wakati itakuja kuleta ajali kubwa sana na ikiwezekana bajeti ya mkoa iongezwe kutokana na tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Serikali itoe kipaumbele kwa barabara zetu za kiuchumi zilizopo katika Mkoa wa Iringa. Kwa sababu tumeona barabara hizi mara nyingi zimekuwa hazipitiki wakati wa mvua na kusababisha karibu siku mbili au tatu magari hayapiti, kwa hiyo, hilo ni tatizo kubwa. Barabara za Mafinga – Mgololo; Kilolo – Idete –Ipalamwa; Kinyanambwa – Saadani – Madibira na Kalenga – Kiponzelo, hizi ni barabara za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna barabara nyingine za kiuchumi ambazo ziko TARURA, pengine kwa sababu TANROADS huwa inachukua barabara za msongamano wa Dar-es-Salaam ingejaribu kuchukua hata barabara ambazo ni za kiuchumi zilizopo katika mkoa wetu ili huu uchumi wa viwanda sasa kwa sababu malighafi ziko huko, itakuwa matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka nichangie kuhusiana na TAZARA. Ni lini Serikali itarekebisha Sheria ile ya TAZARA kwa sababu imeshapitwa sana na wakati na utaona inawa-favour sana Wazambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile TAZARA ina madeni, Serikali ililipa milioni 550 lakini bado wanadai milioni 745. Hivyo, tungetaka tujue lini watawalipa hawa wafanyakazi ili waendelee kuwa na moyo wa kuitumikia Serikali yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niendelee kuzungumza kuhusu USCAF, Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, niwapongeze wamefanya kazi nzuri, hata mimi nilishawahi kwenda katika ziara zao kwa kweli wamepeleka mawasiliano vizuri. Hata hivyo, kuna baadhi ya maeneo katika Mkoa wetu wa Iringa bado ni matatizo. Kuna Lyamungo, Mfukulembe, Kalenga, Mpanga TAZARA, Lulanda, Mlafu, Mahenge, Ilindi, Magana, Iramba, kote huko bado kuna matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu naona iongeze kasi ya usambazaji wa mawasiliano sehemu ambazo hazina mvuto wa kibiashara, lakini pia iongeze rasilimali watu ili hii kazi iweze kwenda kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako na Naibu Waziri kwa kazi nzuri pamoja na kuwasilisha bajeti yao ili tujadili. Yapo mambo ambayo nilikuwa nataka kupatia ufafanuzi na pia kutoa ushauri kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa usambazaji wa vifaa vya elimu kwa shule maalum za watoto wenye ulemavu. Nampongeza Waziri, Mheshimiwa Profesa Ndalichako kwa utaratibu wake wa kuvikagua kama vipo na kama vinatumika. Ni suala zuri sana kwa sababu kuna baadhi ya shule huwa zinapokea vifaa hivyo na kuviacha bila kutumika na wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba kuwepo na utaratibu maalum wa kuwa na Mkaguzi Maalum wa vifaa hivi ili aweze kukagua na kuvifanyia ukarabati. Pia kuna baadhi hawana wataalam wa kufundisha, kwa wale wasiojua kuvitumia hasa walimu wao. Pia walimu katika shule hizi wote wangepatiwa elimu ya mawasiliano kwa watu wasiosikia. Shule hizi pia ziwekewe uzio kama Lugalo iliyopo Iringa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni ukarabati wa shule kongwe. Naipongeza Serikali kwa zoezi la ukarabati wa shule kongwe nchini, kwani shule hizi zilikuwa na miundombinu chakavu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu Bima ya Afya katika Vyuo Vikuu. Nilibahatika kukutana na Serikali za Vyuo Vikuu vilivyopo katika Mkoa wa Iringa. Changamoto yao kubwa ni kuhusiana na Bima ya Afya wanafunzi wanayochangia pesa ya matibabu lakini hawapewi kadi za matibabu kwa sababu vyuo vinakuwa havijapeleka pesa katika mfuko. Ushauri wangu kwa hili, ni vyema Bima ya Afya waweke dawati katika vyuo ili malipo yalipwe moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundombinu chakavu katika vyuo, ni vyema pia Serikali ingekuwa na programu pia ya kuvifanyia ukarabati wa majengo shule hasa mabweni wanayoishi wanavyuo, mfano Chuo cha Mkwawa, mabweni yao hayajakarabatiwa kwa muda mrefu. Pia kuna upungufu wa madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuendelea kukopesha vijana wetu mikopo ya elimu ya juu. Naomba kigezo cha kupatiwa wanafunzi waliosoma katika shule za private, lingekuwa liondolewe kwa sababu kuna wanafunzi ambao ni yatima, wanasomeshwa katika shule hizo kwa ufadhili maalum au kuna wazazi waliokuwa wakati huo ni waajiriwa, lakini baadae wakastaafu uwezo wa kulipia vifaa, wao wanakosa. Pengine Serikali ingeangalia uwezekano wa mikopo hiyo kukopeshwa na taasisi za fedha ili hata kudai au kukusanya mkopo huo unakuwa rahisi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya na kwa kweli wanaombeza labda hao ni wanga tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa pamoja na Naibu wake wote kwa kazi nzuri ambazo wamekuwa wakizifanya katika Wizara hii. Wamezindua miradi mingi sana ukiwepo ununuzi wa ndege na ujenzi wa reli ya umeme, niwapongeze sana. Kutokana na kazi nzuri ambayo reli imekuwa ikifanya kuna ule mfuko wake pengine wangeachiwa maana unachukua muda mrefu na wao wana kazi nyingi na tunajua kwamba tunataka reli hii ikamilike mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niipongeze Serikali kwa ujenzi wa kiwanja cha ndege, mwenzangu amepongeza na mimi napongeza. Kupitia World Bank Kiwanja chetu cha Nduli kitajengwa ikiwa package mojawapo na ile barabara inayokwenda mbuga za wanyama. Kwa kweli naamini kabisa Mkoa wetu wa Iringa sasa tutapata uchumi wa kutosha na utafunguka kiutalii kwa sababu tukishajenga uwanja na tukishapeleka barabara ya lami Ruaha National Park najua kwamba Nyanda za Juu Kusini na Mkoa wa Iringa pia utafunguka kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee kupongeza Serikali kuhusiana na ujenzi wa mtandao wa barabara nchini ikiwepo barabara ya Dodoma - Mtera - Iringa kilometa 260. Kwa kweli barabara hii imekuwa mkombozi sana kwetu, inatufanya dakika dakika mbili tumefika Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ipo changamoto kubwa pale, ningeomba Mheshimiwa Waziri aangalie na ikiwezekana labda twende akaiangalie vizuri zaidi pamoja na wataalam wake. Wakati wa mvua ile barabara mawe yanadondoka kiasi kwamba kuna wakati magari hayapiti kabisa. Kwa hiyo, tumemwona hata Meneja wa TANROARDS, Ndugu Kindole, karibu siku tatu amefanya kazi nzuri sana. Kwa hiyo, naomba kabisa barabara hiyo iangaliwe kwa sababu kuna wakati itakuja kuleta ajali kubwa sana na ikiwezekana bajeti ya mkoa iongezwe kutokana na tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Serikali itoe kipaumbele kwa barabara zetu za kiuchumi zilizopo katika Mkoa wa Iringa. Kwa sababu tumeona barabara hizi mara nyingi zimekuwa hazipitiki wakati wa mvua na kusababisha karibu siku mbili au tatu magari hayapiti, kwa hiyo, hilo ni tatizo kubwa. Barabara za Mafinga – Mgololo; Kilolo – Idete –Ipalamwa; Kinyanambwa – Saadani – Madibira na Kalenga – Kiponzelo, hizi ni barabara za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna barabara nyingine za kiuchumi ambazo ziko TARURA, pengine kwa sababu TANROADS huwa inachukua barabara za msongamano wa Dar-es-Salaam ingejaribu kuchukua hata barabara ambazo ni za kiuchumi zilizopo katika mkoa wetu ili huu uchumi wa viwanda sasa kwa sababu malighafi ziko huko, itakuwa matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka nichangie kuhusiana na TAZARA. Ni lini Serikali itarekebisha Sheria ile ya TAZARA kwa sababu imeshapitwa sana na wakati na utaona inawa-favour sana Wazambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile TAZARA ina madeni, Serikali ililipa milioni 550 lakini bado wanadai milioni 745. Hivyo, tungetaka tujue lini watawalipa hawa wafanyakazi ili waendelee kuwa na moyo wa kuitumikia Serikali yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niendelee kuzungumza kuhusu USCAF, Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, niwapongeze wamefanya kazi nzuri, hata mimi nilishawahi kwenda katika ziara zao kwa kweli wamepeleka mawasiliano vizuri. Hata hivyo, kuna baadhi ya maeneo katika Mkoa wetu wa Iringa bado ni matatizo. Kuna Lyamungo, Mfukulembe, Kalenga, Mpanga TAZARA, Lulanda, Mlafu, Mahenge, Ilindi, Magana, Iramba, kote huko bado kuna matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu naona iongeze kasi ya usambazaji wa mawasiliano sehemu ambazo hazina mvuto wa kibiashara, lakini pia iongeze rasilimali watu ili hii kazi iweze kwenda kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na pongezi kwa Waziri Mheshimiwa Angellah Kairuki; Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Doto Biteko na Mheshimiwa Stanslaus Nyongo; na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na kuwasilisha hotuba yao ili tuweze kuijadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Serikali na kipekee nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuamua kufanyike marekebisho ya Sheria za Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nalipongeza Jeshi la Wananchi kwa ujenzi wa ukuta wa Mererani ambao umeweza hata kupandisha thamani ya madini ya tanzanite.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu elimu katika maeneo ya machimbo. Katika machimbo, wachimbaji wadogo hawana elimu ya kutosha kuhusu hatari zilizopo machimboni. Pia kuna maambukizi makubwa sana ya UKIMWI. Je, ni mkakati gani Serikali inaweka ili kuwanusuru vijana wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia yanapoanzishwa machimbo mapya kama machimbo ya Nyakavangala yaliyopo Jimbo la Ismani Mkoa wa Iringa, ni utaratibu gani unafanywa ili kuwaelimisha wananchi walio katika machimbo ili kujua fursa zilizopo katika eneo lao? Kwa sababu kuna watu wanakuja kutoka maeneo mbalimbali kufuata fursa wakati waliopo katika maeneo hayo wanakuwa hawajui.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika machimbo mapya kuna tatizo kubwa sana la huduma za kijamii kama ulinzi, vyoo, zahanati na kadhalika. Halmashauri hazina uwezo, je, Wizara huwa inawasaidiaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu fedha kutopelekwa katika vyuo vya madini. Vyuo vyetu ya madini vina changamoto kubwa sana ya fedha kutopelekwa kwa wakati. Naomba kama Serikali ina dhamira ya dhati ya kusaidia sekta hii, itoe fedha kwa wakati ili kuboresha vyuo vyetu ili viweze kuwa na mazingira mazuri ya kuzalisha watalaam wetu wa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni watoto wadogo kutumika katika machimbo. Pamoja na kuwa ipo sheria ya kumlinda mtoto kutoajiriwa au kutumika kufanya kazi, lakini tumeona umekuwa ni utaratibu wa baadhi ya wananchi na makampuni kuwatumia watoto wadogo kufanyishwa kazi migodini. Je, hatua gani zinawekwa na Serikali kukomesha tatizo hilo?

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua, je, Serikali inaisaidiaje STAMICO ili kuiwezesha kupata fedha ya kutosha ili shirika hili liweze kufanya kazi yake kama ilivyokusudiwa katika uanzishwaji wake?

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza tena Mheshimiwa Waziri na Manaibu wote. Nina imani kwa juhudi yao watainua sekta hiii ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kumpongeza Waziri wa Maji, Mheshimiwa Engineer Isack Kamwelwe; Naibu Waziri, Mheshimiwa Aweso na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri ya kuwasilisha bajeti hapa Bungeni. Wizara hii ni muhimu sana, lakini bado Serikali haijaweza kuleta pesa ya kutosha katika miradi ya maji nchini. Kuna mtiririko wa fedha za miradi ya maendeleo zilizoidhinishwa na Bunge hazipelekwi kwa wakati katika miradi yake. Nikiwa mmoja wa Mjumbe wa Kamati hii, naomba Serikali izingatie sana maoni ya Kamati na ifanye kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na Kamati ya Bunge na Wabunge wote waliopendekeza kuwa kuwepo na ongezeko la tozo ya shilingi 50 kwa lita ya mafuta ya petroli na dizeli ili kutunisha Mfuko wa Maji kama ilivyo kwa miradi ya barabara na umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema sasa Serikali ikaanzisha Wakala wa Maji Vijijini kama ilivyo Wakala wa Umeme na TARURA. Hii inasaidia kwa haraka miradi iliyopo vijijini, sababu ndiko kwenye matatizo makubwa sana ya maji kuliko mijini. Pia tumeona jinsi hizo Wakala nyingine zilivyoweza kutekeleza kwa haraka na eneo kubwa, toka kuanzishwa kwake, ndiyo maana tunapendekeza kiundwe chombo hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya umwagiliaji ndiyo mkombozi wa maendeleo ya nchi nyingi duniani. Tunatambua kuwa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inahimiza umuhimu wa kuendeleza eneo kubwa lililopo nchini linalofaa kwa umwagiliaji kwa kuweka miundombinu ya umwagiliaji kwa ajili ya kuongeza tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo, kwenye maeneo ya chakula, biashara, malisho na kilimo cha majani. Halmashauri nyingi sana zikiwemo Halmashauri zilizopo katika Mkoa wa Iringa, zinajenga miradi ya umwagiliaji kwa kuanza na kutumia pesa za Halmashauri. Miradi mingi sana inachelewa kukamilika kutokana na ucheleweshwaji wa pesa za miradi hiyo toka Serikalini (Wizarani).

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na wingi wa miradi hiyo, nilikuwa napenda kujua, je, Serikali huwa inatumia vigezo gani kupeleka pesa hiyo katika miradi ya umwagiliaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Meneja wa IRUWASA katika Mkoa wetu wa Iringa, amekuwa akisimamia miradi vizuri sana na kusababisha upatikanaji wa maji katika Manispaa ni asilimia 96. Tatizo lililopo ni mji kupanuliwa kwa haraka sana na Mkoa unahitaji sasa kupata mabomba makubwa ya kusambaza maji katika maeneo yote kwa wakati, kwa sababu yaliyopo sasa hivi hayatoshelezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri alipotembelea katika Mkoa wetu, kwani alitoa semina ambayo alitujengea uwezo mzuri sana wa kufuatilia pesa za miradi ya umwagiliaji. Pia uamuzi wa IRUWASA kusimamia miradi ya Mkoa wa Iringa ni la busara sana. Pia naipongeze Serikali kwa kusaini pesa za mradi mdogo wa maji Ilula, Jimbo la Kilolo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na changamoto kubwa sana ya usambazaji maji safi na salama na hasa kulikuwa na yale mabomba ya Mchina ambayo yalikuwa ni tatizo. Nawapongeza angalau kwa sasa wameweza kujitahidi kwa kiasi kikubwa sana kuweza kusambaza maji hata maeneo mengi. Pia nampongeza sana Meneja wa DAWASCO lakini naomba kasi iongezeke.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto kubwa sana katika shule zetu za msingi na sekondari hasa kuhusiana na elimu bure. Hakuna michango yoyote inayotolewa shuleni kwa ajili ya tozo za maji na umeme. Hivyo kufanya shule nyingi kukatiwa maji na kusababisha mlipuko wa magonjwa na watoto wetu kusoma katika mazingira magumu sana. Hivyo, naiomba Serikali jambo hili ilipime na ichukue maamuzi kama ilivyo kutoa elimu bure na tozo za maji ziondolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali itatoa elimu kwa wananchi juu ya uvunaji wa maji? Kwa sababu kumekuwa na kipindi kirefu cha mvua na kusababisha mafuriko na uharibifu wa mazingira; ni kwa nini Serikali isitumie mvua, hivyo kutoa elimu ili wananchi wavune maji na yatumike wakati wa kiangazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumpongeza Waziri wa Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora, Mheshimiwa Capt. Mkuchika; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa; Makatibu wote wawili na Watendaji wa Wizara hii kwa kazi nzuri sana wanayoifanya na pia kwa kuwasilisha hotuba yao hapa ili tuweze kuijadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mkurugenzi wa TASAF kwa kazi nzuri aliyofanya katika Mkoa wetu wa Iringa. TASAF imefanya vizuri sana, imeweza kusababisha hali ya kaya masikini na kuwa na hali zenye unafuu wa maisha japokuwa mwanzoni kulikuwa na ukiritimba katika kuzibaini. Kuna baadhi ya watendaji walitaka kutumia kisiasa kaya za watu masikini na walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Waziri wa Utumishi Mheshimiwa Capt. Mkuchika kwa kuitembelea kaya masikini na yenye watoto walemavu zaidi ya watatu inayoishi katika Kijiji cha Lulami na kujionea jinsi ilivyo na kuiongezea kipato na kuipatia TV. Nilikuwa naomba kujua: Je, kaya masikini na yenye watoto wenye ulemavu kama hiyo, Serikali inawasaidiaje kuwapatia angalau mradi endelevu unaoweza kusaidia watoto wenye ulemavu kama hao ambao hawana hata uwezo wa kutembea kabisa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na tatizo kubwa sana la upandishwaji wa madaraja kwa Walimu na wanapopandishwa marekebisho ya mishahara hayafanyiki kwa wakati na kusababisha mpaka wakati mwingine Mwalimu anastaafu lakini mshahara wake unakuwa haujarekebishwa. Je, nini mkakati wa Serikali kwa changamoto kama hiyo? Hii inasababisha usumbufu mkubwa sana kwa wastaafu ikiwa ni pamoja na ucheleweshaji wa mafao yao wanapostaafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa sana kwa wafanyakazi wanapokaimu nafasi kuthibitishwa. Je, sheria inasemaje ili kumpatia haki mtu anapokaimu kwa muda mrefu?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. John Tizeba, Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri. Nampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara zake nyingi zilizoleta tija kwa ajili ya kilimo chetu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 75 ya wananchi wanaishi vijijini na asilimia 65 ni wakulima na wanategemea kilimo, lakini bado Serikali haijaweza kuwa na mkakati wa kumsaidia mkulima. Yapo mambo ambayo ningeomba kupata ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Kilimo ilianzishwa ili kuweza kumsaidia mkulima mtaji kwa sababu wakulima hawakopesheki. Pamoja na benki hii kuwa Dar es Salaam, bado Serikali haijaweza kuweka pesa ya kutosha kwa ajili ya kukopeshwa wakulima. Kwa ushauri wangu benki hii makao makuu yahamie Dodoma, lakini kuwepo na matawi kila kanda ili wananchi waweze kuwafikia kwa urahisi. Ushauri wangu ni kwamba Serikali iongeze mtaji katika benki hiyo ili ibebe jukumu la kutoa mikopo kwa wakulima wengi na yenye riba nafuu ili kilimo kiwe na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu pesa ya utafiti 1% ya bajeti, ni lini Serikali itatenga pesa ya kutosha kwa ajili ya watafiti ili wataalam wetu waweze kufanya tafiti mbalimbali hasa za mbegu, mbolea hata waweze kupima udongo wa maeneo mbalimbali ili wakulima wetu walime kilimo chenye tija na cha uhakika kuliko sasa hivi ambapo mkulima analima kilimo cha kubahatisha, hana uhakika na kilimo chake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenendo huu unadhihirisha kukosekana kwa dhamira ya dhati ya uwekezaji katika miradi ya kilimo na kikwazo katika ukuaji wa kilimo na kupunguza umasikini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani wanafanya kazi gani katika maeneo yao? Mbona wakulima wetu hawana elimu ya kutosha ya kilimo ya kueleweshwa kuhusu mbegu bora, utumiaji wa mbolea na matumizi ya ardhi kwa ujumla? Ni kwa nini yasianzishwe mashamba darasa katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kusaidia kuwapatia elimu wakulima wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu alipofanya ziara Iringa alitueleza kuwa NSSF wameamua kufufua kinu cha kusaga mahindi cha Iringa (National Milling) kwa ajili ya kuleta tija kwa wakulima wetu wa Mkoa wa Iringa. Sasa je, huo mpango bado upo? Sababu kinu hiki kilikuwa kinaleta ajira, pia ni soko hata kwa wakulima wetu la mahindi. Wakulima nchini hasa wa Mkoa wa Iringa wanapata shida sana kwa sababu upatikanaji wa mbolea katika maeneo mbalimbali haukidhi mahitaji ya wakulima nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia zipo changamoto nyingi sana zikiwemo za wasambazaji mbolea kwamba hawazingatii kabisa bei elekezi za Serikali na kusababisha bei ya mbolea kuwa kubwa sana, mbolea haifiki kwa wakati, hawazingatii msimu unaanza lini na kadhalika. Ni kwa nini Serikali isiangalie uwezekano wa kuondoa tozo katika mbolea ili bei ya mbolea ipungue?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali izingatie ushauri wa Kamati. Kamati imeshauri mambo mengi sana ambayo kama yakizingatiwa yanaweza kusaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Tanzania tumekuwa na kilimo cha kubahatisha na wakulima wengi wanategemea kilimo cha mvua na msimu wake hautabiriki, ni lini Serikali itaanzisha Bima ya Kilimo ili wakulima waweze kukopesheka kuliko ilivyo sasa mkulima hakopesheki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Balozi Dkt. Mahiga, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na kuweza kuwasilisha hotuba yake hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo masuala ambayo naomba kupatiwa ufafanuzi, ambayo ni haya yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, sheria zilizopitwa na wakati; kumekuwa na malalmiko mengi kuhusiana na Sheria nyingi kupitwa na wakati na kusababisha wananchi kutotendewa haki. Je, kuna utaratibu au mkakati gani ili kuhakikisha kuwa zile sheria zilizopitwa na wakati, Miswada inaletwa Bungeni ili kuzifanyia marekebisho au kuhuishwa.

Pili, hukumu kuandikwa katika lugha ya Kiingereza; naomba kujua ni kwa nini Serikali haijaweza kuweka utaratibu wa hukumu kuandikwa kwa lugha ya Kiswahili na kutenda haki kwa mshtakiwa kukata rufaa? Kwa sababu nilipotembelea gereza kuu Mkoa wa Iringa changamoto mojawapo ya wafungwa ilikuwa wameshindwa kukata rufaa kutokana na kutoelewa lugha iliyoandikwa na hasa kama huna Mwanasheria wa kukusaidia. Je, Serikali haioni kama hawatendi haki kwa wasiojua lugha ya Kiingereza? Naomba kujua mkakati wa Serikali kuhusiana na hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wa mashtaka; naomba kujua umri wa mashtaka kwa sababu ipo kesi ya waliokuwa wafanyakazi wa kilichokuwa Kiwanda cha Kukata Almasi (Tancut Diamond Iringa), kiwanda kilifungwa mwaka 1995 kwa kuingia mufilisi, hivyo wafanyakazi hawajalipwa na toka wakati huo walifungua kesi dhidi ya Serikali lakini matokeo yake mpaka leo bado wanaendelea kuhudhuria mahakamani. Naomba ufafanuzi juu ya suala hilo kwa sababu linachukua muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa kutoa tamko la kumaliza mashtaka yanayohusu wanawake na watoto ndani ya miezi sita. Kwa hili napongeza sana, sababu katika Mkoa wetu wa Iringa kumekuwa na kesi nyingi za ubakaji watoto ambao zimechukua muda mrefu sana kwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Hamisi Kigwangalla (Mb), Naibu Waziri Mheshimiwa Hasunga na watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba yao ya bajeti ili tuweze kuijadili. Nimpongeze Waziri kwa kuongeza pato la Taifa kwa zaidi ya asilimia tano, hongera sana.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa ujenzi wa viwanja vya ndege nchini kikiwamo Kiwanja cha Ndege cha Nduli, Mkoa wa Iringa. Pia ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami inakwenda katika Hifadhi ya Ruaha. Tunaamini kabisa miundombinu itakapokamilika Mkoa wa Iringa utakuwa kitovu cha utalii, pia Nyanda za Juu Kusini kutafunguka kiutalii na pato la mkoa na nchi litaongezeka.

Mheshimiwa Spika, kuvibaini vivutio zaidi vya utalii vilivyoko nchini na kuviendeleza, nilikuwa naomba Serikali itueleze mpango maalum walioupanga kwa ajili ya kuvibaini vivutio vilivyopo katika nchi yetu kwa ajili ya kuiendeleza na kuvitangaza ili viwe na tija na visaidie kuongeza pato la Taifa. Katika Mkoa wetu wa Iringa kuna vivutio vingi sana vya utalii ambavyo bado havijapewa kipaumbele katika kuvitangaza kama vile Fuvu la Kichwa cha Mkwawa, Jiwe la Hangilongo (jiwe lililokuwa linaongea), sehemu waliyokuwa wananyongwa watumwa (vitani), sehemu waliyopigania uhuru alipokuwa anaishi Mandela, Lugalo sehemu lilipo kaburi la Nyundo na vingine vingi sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu elimu ya utalii, nilikuwa pia nataka kujua mpango mkakakti wa kuwapatia elimu wananchi wa Mkoa wa Iringa. Tunaipongeza Serikali kwa uzinduzi wa utalii katika mkoa wetu kama kitovu cha utalii wa Nyanda za Juu Kusini. Ni imani yangu kabisa kupitia utalii wananchi wetu watajiajiri. Kama wataandaliwa katika utalii kuna ajira nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa ununuzi wa ndege ambazo nina imani utaongeza utalii katika mikoa yetu na nchi yetu. Tulikuwa tunaomba huu mradi wa Regrow unaokuja kukuza utalii Nyanda za Juu Kusini uendelee kusaidia utangazaji wa vivutio vya utalii vilivyopo katika mikoa hii ya Kusini. Mradi huu uendelee ku-support maonesho haya yaliyozinduliwa Iringa ya Karibu Kusini ambapo imefanyika kwa miaka miwili kwa Mikoa ya Iringa, Mbeya, Njombe, Songwe, Katavi, Ruvuma na Rulewa.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru mradi huu utajenga jengo kama Kituo cha Utalii eneo la uliokuwa Msitu wa Kihesa, Kilolo Iringa. Nilikuwa naomba watakapojibu watujulishe makao makuu ya mradi huu ni wapi? Kwa kuwa mradi wa Spanest unaishia mwezi wa sita, je, utaongezewa muda tena? Kwa kuwa sasa mkoa wetu utakuwa kitovu cha utalii, je, Serikali imejiandaaje kutoa elimu na mafunzo kwa wananchi ili waweze kujiajiri kupitia utalii?

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Iringa una eneo la uwekezaji lililopo katika Msitu wa Kihesa, Kilolo ekari 640 za eneo zima, lakini ekari 230 Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ilipatiwa kuendeleza katika utalii. Tunaomba Serikali ilete rasilimali fedha na rasiliamali watu ili kusaidia kuutunza msitu huo kwa eneo lililobaki.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mkoa wa Iringa katika Halmashauri zote kuna vivutio vya utalii, pamoja na kuwa Afisa Wanyapori, Dada Hawa Mwechaga anafanya kazi nzuri sana za utalii pia Mkuu wetu wa Mkoa Mheshimiwa Amina Masenza anahamasisha sana utalii, tunaomba Wizara ya Maliasili na Utalii ishirikiane na Wizara ya TAMISEMI ili kuhakikisha Halmashauri inakuwa na Afisa Utalii ili vivutio vilivyomo katika Halmashauri zetu vitumike kama vyanzo vya mapato. Niendelee kumpongeza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mito yenye mamba, niendelee kumpongeza, naomba kujua Serikali inasaidiaje mito yenye mamba hasa katika Mkoa wa Iringa? Wanasaidiwe kuvuta maji ili wananchi wasiendelee kuuawa na kupata ulemavu?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na pongezi nyingi sana kwa Waziri Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe, Naibu Waziri, Mheshimiwa Juliana Shonza na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuinua vipaji na kuendeleza soka la Tanzania pamoja hotuba yao iliyowasilishwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mazuri yaliyoorodheshwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nilikuwa naomba nipatiwe ufafanuzi wa mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ripoti nyingi sana za mchakato wa Vazi la Taifa na tumekuwa na kiu kubwa sana kuona mchakato huo unafika mwisho ili Tanzania itambulike kwa vazi lake kama zilivyo nchi nyingine. Je, ni lini sasa Serikali itahitimisha hili jambo zuri?

Mheshimiwa Spika, vijana wetu wa kike wamekuwa wakishiriki Mashindano ya Ligi (soka) Timu za Wanawake, wakiwa na changamoto nyingi sana kiasi kwamba hata ushiriki wao umekuwa mgumu. Nilitegemea ligi hii ingetumika hata kupata vipaji kwa mabinti zetu ili waweze kushiriki katika Timu ya Taifa ya wanawake.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua mkakati wa Serikali wa kusaidia hizi Timu ziweze kushirihiki ligi kuu, kwa sababu wanaishi katika mazingira magumu mpaka wanadhalilishwa kwa kutembeza mno bakuli.

Mheshimiwa Spika, nashirikiana na wote walioipongeza TBC kwa kazi nzuri sana. Nilikuwa naiomba Serikali itoe kipaumbele kuongeza bajeti ili waboreshe mitambo, pia usikivu uwepo katika maeneo yote kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu vilevile nianze kutoa pole nyingi sana kwa wananchi wa Iringa kwa msiba mzito ambao tumepata kuondokewa na watoto wetu wapenzi Maria na Consolatha ni watoto ambao wametupa elimu kubwa sana na wametufundisha funzo kubwa sana, tunaomba Mwenyezi Mungu awapokee na awalaze mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mpango vilevile nimpongeze Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Kijaji na ni wapongeze Wakurugenzi wote au watendaji wote wa taasisi za fedha kwa kazi nzuri wanazozifanya.

Nianze mchango wangu kwanza kuongelea kuhusu ucheleweshaji wa fedha katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ucheleweshaji wa fedha katika halmashauri zetu za maendeleo umefanya miradi mingi sana kutokamilika kwa wakati hivyo ningeiomba Serikali ingejaribu kuangalia ile miradi ambayo ina tija pesa ingeletwa kwa wakati. Kwa mfano nikitoa tu mfano katika Halmashauri yangu Manispaa ya Iringa Mjini kuna mradi ambao ni wa machinjio wa Ngerewala huu mradi umeanza toka mwaka 2008 na huu mradi tulikuwa tunaimani kabisa kama ungeletewa fedha kwa wakati ungeweza kusaidia hata miradi mingine na ni chanzo kizuri sana cha mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ungeweza ukatoa ajira kubwa sana katika Manispaa yetu hivyo ningeomba Serikali ingekuwa inajaribu kuangalia kufanya upembuzi yakinifu wa miradi ile ambayo unajua ina tija ambayo inaweza ikasaidia ikaweza kuletewa pesa nzuri zaidi huwa sielewi kama Serikali huwa inatumia vigezo gani kutenga hizi fedha katika hii miradi ya maendeleo. Sasa ni vizuri sana Serikali ingetenga fedha kukamilisha miradi kama hii ili tuweze kupata chanzo kikubwa cha Halmashauri zetu na vile tungeweza kukusanya pesa nyingi katika kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ninaomba nizungumzie kuhusiana na madeni ya wazabuni. Kuna wazabuni wanaidai Serikali hii kwa mda mrefu sana toka mwaka 2012 wako wengi sana wanadai Serikali yetu. Nakumbuka Mheshimiwa Rais pia aliwahi kuagiza kwamba wazabuni wote walipwe pesa zao sasa sijajua kama walilipwa na utaratibu gani ulitumika kwasababu bado kuna malalamiko mengi sana kwa wazabuni kutolipwa pesa zao. Na kumbuka kwamba kuna wazabuni wengi sana walikuwa wamekopa benki na kuna wazabuni wengine wameuziwa mali zao kutokana na riba kubwa ambazo walikuwa wanadaiwa na benki. Kwa hiyo, ni vizuri labda Serikali ingealia na vilevile tunaona kwamba hawa wazabuni pia bado walikuwa wanatozwa na TRA kwamba wanahesabika kama wamefanya biashara na wakati bado hawajalipwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa labda kungekuwa na utaratibu mzuri wa kuangalia kudai hata hizi VAT ambazo wazabuni wanadai Serikali, wangeangalia hata sheria iwalinde kwa sababu bado wanakuwa wanadaiwa na Serikali, bado wao wanaidai Serikali sasa ningeomba labda uangalie utaratibu hata ile Sheria ya VAT. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusu sekta ya mazao ya misitu kama mbao, mirunda, nguzo ambazo kwa kweli ndio biashara kubwa ambayo inafanyika katika Mkoa wetu wa Iringa na hata Njombe na sehemu nyingine. Huu utaratibu wa kudai risiti za EFD wakati wa kusafirisha mazao haya kwenye maroli umekuwa ni kero kubwa sana kwa wafanyabiashara kumbuka mazao haya mkulima anakuwa anasafirisha anapeleka sokoni ndipo alipwe lakini sasa anapodaiwa hizi risiti hata wale wasafirishaji wale wa maroli wanakuwa wanakata kubeba mizigo yao. Kwa hiyo, inasababisha sasa mfanyabiashara wa roli hapati pesa hafanyi biashara, mfanyabiashara wa mbao hafanyi biashara hata kuna vijana wanasaidia kupakia hizi mbao hawapati pesa. Kwa hiyo, pengine ningomba sasa ingetafutwa utaratibu mzuri wakusanye hizi pesa za mazao ya mbao ambayo wafanyabiashara imekuwa ni kero kubwa sana katika Mkoa wetu wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze sana Kamishna Mkuu wa TRA Mr. Kichele tumemuona katika vyombo vya habari anazunguka nchi nzima, anapita kwenye maduka, anakagua, sasa huwa najiuliza na anakuta kuna madudu mengi sana. Sasa hawa maafisa walio katika hii mikoa ina maana hawapiti kuona haya madudu ambayo Kamishna anayaona labda ni vizuri sasa na wao wakajaribu sasa kupita na kuangalia kuliko wamsubiri Kamshina Mkuu ndio anakuja kugundua madudu ambayo yapo.

Mheshimiwa Spika, pia nizungumzie kuhusiana na wafanyabiashara wadogo na kodi, ningeomba labda Serikali ingekuwa na utaratibu wa kila mwaka unapoanza TRA kupitia idara yao ya elimu kwa mlipa kodi wangekuwa kuna elimu wanawapatia na pia wawasilikilize kero au wasikilize hoja zao na lugha pia iwe rafiki kwa wafanyabiashara kwa sababu naona lugha sio nzuri sana maafisa wetu wa TRA wanapokwenda kukusanya hizo kodi wanatishiwa wanawekewa kodi ambazo siyo, kwa hiyo mfanyabiashara anakuwa anakata tamaa sana na biashara anapoanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ningeomba Serikali kuwepo na utaratibu wa kuwasaidia hawa wafanyabiashara wadogo hata ikiwezekana wanapoanza hizi biashara basi angalau kodi wasianze na kodi kubwa kwa sababu unakuta wanatozwa kodi hata biashara hawajafanya. Lakini kungekuwa na utaratibu mzuri kama nchi za wenzetu, kwamba wanawasaidia wanaanza kuwapa pesa wanaanza kuwatoza kodi kidogo hata asilimia 10 halafu baadae inapanda kidogo kidogo watakuwa wanawajengea utaratibu mzuri kwanza wigo mpana wa kodi utaonekana kwa sababu wafanyabiashara wengi sana watasajili, watalipa kodi na vilevile itasaidia Serikali kukusanya kodi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nizungumzie kuhusu tariff ya East Africa Community. Tanzania na wenyewe wawe wepesi kubadilika kutokana na tozo ambazo zimekuwa zikibadilika badilika. Kwa sababu tunaona nchi nyingine kwa mfano Kenya au Uganda kuna tariff ambazo wanakuwa wanazitoa yaani kodi zile zinaondolewa tozo. Lakini unaona Tanzania kutotoa zile tozo mapema sasa hata biashara zinaondoka, watu badala ya kwenda kupitisha hata biashara kwenye bandari yetu unakuta wanapitisha kwenye bandari nyingine kwa sababu tayari tozo zinakuwa zimeondolewa pengine kwa sababu ni biashara ya East Africa basi kuwepo na utaratibu mzuri wenzetu wakiondoa na sisi tuondoe ili na sisi tuweze kupata biashara nzuri zaidi kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusu wafanyabiashara wanaodaiwa madeni na TRA kwa miaka ya nyuma. Kumekuwa na utaratibu sasa hivi wa maduka mengi sana yamefungwa hasa pale Iringa, kwamba kuna madeni wanadaiwa ya nyuma na utakuta pengine walikuwa wamekisiwa tofauti yaani hawakukisiwa inavyotakiwa. Sasa unaona miaka 10/miaka mitano bado mfanyabiashara yule anashindwa kulipa madeni, labda kungekuwepo na utaratibu kwamba badala ya kuwafungia maduka basi wawaachie wawe wawalipa kidogo kidogo kwa sababu wakifungia bado Serikali inakosa kodi. Lakini wakiwaachia wakalipa kidogo basi angalau inasaidia wao wanapata biashara zinaendelea na Serikali inaendelea kupata zile kodi.

Mheshimiwa Spika, tungefanya labda utaratibu kama tulivyofanya zile tozo za magari kwamba walizifuta zile za nyuma zote tukaanza upya pengine ipo haja kwa sababu utakuta hawa wafanyabiashara wengi wao walikadiriwa kodi ambayo haikuwa ya ukweli kwa hiyo bado wanaendelea kuteswa wanafunga maduka yao. Sasa Serikali iangalie na itoe uzito kwasababu maduka yote yakifungwa maana yake sawa sawa na ng’ombe sasa kama tukimchinja hatupati tena maziwa lakini kama ng’ombe wako ukimpa mashudu unaweza kuendelea kukamua vizuri zaidi. Kwa hiyo, tukiendelea kuwasaidia wafanyabiashara wetu wakafanya biashara zao vizuri, wakawapa elimu nzuri, tutaendelea kukusanya kodi nyingi zaidi na wafanyabiashara wengi sana watafungua biashara, kwa hiyo Serikali itaendelea kupata kodi kwa wingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti yetu ya Serikali. Kwanza, naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia naomba nimpongeze Mheshimiwa Spika na niwapongeze Chama cha Wabunge Wanawake walioko hapa Bungeni kwa hafla hii ya leo ya kuhakikisha kwamba wanahamasisha wananchi kuchangia tukio hilo la kujenga vyoo vya watoto wa kike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu sasa kwa kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Kijaji na Watendaji wote wa Wizara. Pia naipongeza Kamati ya Bajeti ambayo kwa kweli imekuwa ikifanya kazi nzuri sana kuhakikisha bajeti zetu zinakuwa rahisi hata kuzijadili hapa Bungeni. Vile vile bajeti hii ni nzuri sana. Bajeti ambayo ilisomwa tarehe 14 Juni, 2018 ni nzuri sana kwa sababu hata Mwenyekiti wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Mbowe aliipongeza bajeti hii. Kwa hiyo, inaonesha jinsi gani ambavyo bajeti hii imekuwa nzuri. Hata Mbunge wetu wa Iringa alipongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii inatakiwa sasa Watendaji wajipange kuhakikisha yale mambo ambayo yako katika bajeti wanayafanya vizuri ili kusiwepo na malalamiko. Maana Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia, hasa kwenye bajeti ya Serikali kwa Wizara ya Fedha kulikuwa kuna malalamiko mengi sana hasa kwa upande wa kodi. Kwa hiyo, naomba kabisa Mheshimiwa Dkt. Mpango ahakikishe anasimamia bajeti ili wananchi wetu waweze kutendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naungana na Waheshimiwa Wabunge wote waliopongeza Serikali kwa kuondoa ushuru katika taulo za kike. Tatizo hili kwa kweli limekuwa likisumbua sana watoto wetu wa kike na nafikiri lilizungumziwa sana na Wabunge wengi wanawake na huu ulikuwa mshikamano halisi kwamba wanawake wote ni lazima tuhakikishe kwamba tunaipigania hii kodi. Serikali yetu kwa sababu ni sikivu, naona wameiondoa kodi. Kwa hiyo, nina imani kabisa bei zitapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile niendelee kuipongeza Serikali kwa kuondoa kodi katika mikopo inayotolewa katika Halmashauri zetu, ile 5% ya wanawake na asilimia tano ya vijana. Najua kuondoa kodi kutasaidia sana kuwajengea uwezo hasa wa kifedha akinamama na vijana katika Halmashauri zetu kuhakikisha kwamba kile kilio kwamba wanakosa mitaji sasa angalau kwa kuondoa ile kodi watakuwa na mitaji ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba labda Serikali ingeweka wazi kuhusiana na watu wenye ulemavu, kwa sababu hii 5% ya wanawake na vijana bado haijatamka wazi kuhusiana na watu wenye ulemavu katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Manispaa yetu ya Iringa, tayari imetenga 2% kwa kuwakopesha watu wenye ulemavu na vikundi vinne vimepata mikopo ya shilingi milioni tisa. Kwa hiyo, ni jambo zuri. Pengine nchi nzima kungekuwa kuna tengeo la 2% kwa watu wenye ulemavu. Kwa sababu watu wenye ulemavu wamekuwa wakifanya biashara nzuri tu ambapo kwa kweli hawataki kuomba. Ni watu ambao wanaweza kufanya biashara nzuri kuliko hata watu ambao hawana ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee kuhusiana na kilimo. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kilimo, Maji na Mifugo. Uchumi wa Viwanda ambao ndio mwelekeo wa Serikali yetu hii ya Awamu ya Tano unategemea sana sana kilimo. Naipongeza Serikali sana kwa kuweka kilimo kama kipaumbele katika bajeti yetu. Pia Azimio la Maputo linasema asilimia 10 ya mapato ya bajeti ya Serikali ni kwa ajili ya kilimo, lakini karibu miaka mitatu sasa hivi, tunaona kilimo bado hakijapewa kipaumbele. Tunaona hata asilimia moja haitengwi kwa ajili ya kilimo. Kwa hiyo, naiomba Serikali yetu, ili sera yetu ya viwanda iweze kwenda vizuri, ni muhimu sana kutoa kipaumbele katika kilimo nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Serikali ihamasishe sana wakulima wakubwa waweze kuwekeza katika kilimo. Watakapowekeza katika kilimo maana yake hata ajira pia kwa vijana itapatikana kuhusiana na kilimo kwa wakulima wakubwa kama zilivyo nchi nyingine. Vile vile tuwajengee uwezo wakulima wadogo wadogo na kuwawezesha ili kilimo kiweze kuwasaidia, kwa sababu asilimia kubwa sana ya Watanzania ni wakulima wakiwepo watu wa Mkoa wangu wa Iringa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali yetu ijitahidi sana kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji, kwa sababu programu zake nyingi sana za umwagiliaji hazijaweza kufanyika vizuri sana katika maeneo mengi. Unaona maeneo mengi yametengwa, lakini bado kilimo cha umwagiliaji hakifanyi vizuri sana. Ninao mfano halisi kabisa hata katika Mkoa wangu wa Iringa, miradi mingi ya umwagiliaji haijaweza kufanya vizuri kuwasaidia wananchi wanaofanya kilimo. Kwa hiyo, naiomba Serikali yetu ihakikishe kwamba programu za umwagiliaji zinapewa kipaumbe kwa sababu zenyewe hata bila mvua bado tutaendelea kupata mazao mazuri ambayo yatasaidia hata katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu Benki ya Kilimo. Nilitegemea Benki ya Kilimo ndiyo ingekuwa mkombozi kwa wakulima, lakini badala yake inafanya biashara ya kukopesha benki. Maneno haya hata siku ile Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli aliyazungumza wakati wa uzinduzi wa ASDP II. Sasa niombe Serikali isimamie kuhakikisha Benki ya Kilimo inawafikia wakulima na inawakopesha na wakulima waweze kukopesheka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya ziara kwenye Mkoa wa Iringa kwenye miradi hii ya SAGCOT. Tumeona miradi ya SAGCOT ni mizuri sana, lakini kuna changamoto nyingi sana katika baadhi ya viwanda tulivyovitembelea. Kwa mfano, kuna suala la vifungashio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikwenda pale Tanzanice Station pale Njombe, vifungashio ni tatizo kubwa sana. Vifungashio vinanunuliwa kutoka Kenya, halafu sasa kuna walanguzi wanakuja hapa nchini wanachukua mazao, wanapeleka Kenya kwenda kufungasha. Inaonekana kama mazao ni ya Wakenya wakati ni ya Watanzania. Kwa hiyo, ni muhimu sana kuwasaidia watu watakaofungua viwanda vya vifungashio ili kuondoa hii changamoto ambayo iko kwa wajasiriamali wetu na wafanyabiashara wengi waliopo nchini ili kusaidia kuongeza kipato kikubwa katika bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulienda katika kiwanda cha Asasi, tuliona kwamba kimeanza kuwekeza katika vifungashio. Sasa labda kiwezeshwe ili kisaidie kuondoa hii changamoto kubwa ambayo ipo. Kwa sababu pia kuna changamoto tuliona katika Kiwanda cha Silverland na hata Asasi kwamba kuna tozo nyingi sana zinatozwa katika viwanda vyetu, karibu tozo 12 na kusababisha sasa hata wenye viwanda wanakata tamaa. Kwa sababu naona kuna tozo nyingine zinafanana. Kwa hiyo, naiomba Serikali ijaribu kujumuisha hizi tozo iwe moja ili kusaidia watu wengi sana waweze kuwekeza katika viwanda, itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu miradi ya maji, bado mingi haijakamilika na miundombinu yake bado haifanyi kazi, hata iliyokamilika bado haifanyi vizuri. Sasa ile Sh.50/= naona kama Serikali ingeifanyia kazi. Tunategemea kama tutapitisha hiyo Sh.50/=, naona Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamechangia, ingeweza kusaidia sana katika kuhakikisha kwamba mwanamke tunamtua ndoo ya maji kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusu kuhusu miradi ya PPP. Hii miradi ni muhimu sana. Tukichukulia tu mfano wa Daraja la Kigamboni; daraja hili sasa hivi tumeweza kujenga kwa kutumia...

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali twende na mpango huu wa PPP. Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nizungumzie kuhusu ni Electronic Tax Stamp.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja. Naomba Watendaji wote waitendee haki bajeti yetu kwa sababu ni bajeti nzuri sana ambayo tunategemea kwamba itatendea haki hata Chama chetu cha Mapinduzi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu na nitoe pongezi sana kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimwia Dkt. Mwigulu, Naibu Waziri na pia nimpongeze IGP Sirro na Makamanda wote bila kumsahau Kamanda wa Uhamiaji, dada yetu Kamanda Anna Makakala, mwanamke mwenzetu kwa kazi ambazo wamekuwa wakizifanya kulitumikia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu ambaye alikuwa Iringa kwa siku tano. Amefanya kazi nzuri sana na niseme kwamba wananchi wa Iringa kwa kweli wametambua uwepo wake na wametambua kazi nzuri ambazo amekuwa akizifanya kwa wananchi wetu. Nimpongeze sana RPC wa Mkoa wa Iringa, Kamanda Bwire kwa kuhakikisha kwamba usalama umekuwepo kwa kipindi chote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara ya kwanza naomba kumpongeza sana Mchungaji Msigwa, narudia tena, nampongeza sana Mchungaji Msigwa, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini kwa kutambua kazi nzuri ambazo zinafanyika kwa Serikali hii ya Awamu ya Tano na kumtambua kwamba Mheshimiwa Rais, Dkt. Pombe Magufuli anafanya kazi bila kubagua, bila ubaguzi na maneno haya mazuri ameyaongea mbele ya Waziri wetu, Mheshimiwa Jenista Mhagama, mbele ya Mheshimiwa Susan Mgonukulima na Wabunge na wananchi wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nasema sasa Mheshimiwa Msigwa ameanza kukomaa kisiasa. Nashindwa kushangaa, Wabunge wengine wa Upinzani wanapokutana na Rais waseme haya maneno, wamwambie ukweli, lakini wanapoingia humu ndani kwenye Bunge wanaanza kusema tofauti, sasa huo unakuwa unafiki. Hata jana eti wanasema kwamba Rais wetu hakosolewi, mbona mkikutana sasa hamumkosoi? Mnasubiri mpaka muingie humu Bungeni muanze kukosoa, muanze kutukana, mnataka kiki au mnataka nini? Jamani mimi nawaombeni, upinzani wa kweli ni kusema ukweli lakini upinzani wa kweli siyo kuanza kusema vitu ambavyo siyo vya ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nianze mchango wangu;, nizungumzie changamoto ambazo ziko katika Mkoa wa Iringa. Mkoa wa Iringa una changamoto kwa kweli, askari wetu wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana, lakini bado wanaishi kwenye makazi duni. Haya maneno tumeshayazungumza muda mrefu, askari bado nyumba zao siyo nzuri sana kuanzia Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Jeshi la Zimamoto bado hawajaweza kujengewa nyumba nzuri kama ambavyo zilivyo za wanajeshi wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeiomba Serikali yetu kwa kazi nzuri ambazo zimekuwa zikifanywa na askari wetu, basi wajengewe makazi ambayo yanalingana na kazi zao kwa sababu tunapozungumzia makazi pia tunamzungumzia na yule mwanamke ya wale watoto ambao wanaishi kwenye zile nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Serikali hii ingalie umuhimu wa askari wetu kwa kuwajengea nyumba nzuri kwa sababu nyumba ambazo ziko pale Kihesa, mimi nakaa pale Kihesa, ni nyumba ambazo zimejengwa muda mrefu sana, zingeweza zikabomolewa, zikajenga maghorofa kama ambavyo zimejengwa kwenye sehemu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia OC zao za Mkoa wetu bado zinatakiwa ziletwe za kutosha. Stahiki zao zilipwe mara moja kwa sababu wamekuwa wakidai kwa muda mrefu. Upandishaji wa madaraja na vyeo jamani uende kwa muda, wapandishwe kwa muda kwa sababu askari wetu nao wanahitaji wapate stahiki zao. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, lakini nizungumzie Jeshi la Zimamoto, Jeshi la Zimamoto wenzangu wengi wameshalizungumzia nimpongeze Kamanda Andengenye, lakini askari wetu wa Iringa, Kamanda wetu James anafanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Wana vituo vitano vya zimamoto lakini kuna gari moja tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Iringa una uwanja wa ndege, Mkoa wa Iringa una misitu kule Mufindi, kule Kilolo ambapo mara kwa mara ajali za moto zinatokea lakini magari yao ni mabovu sana. Kuna mlima ule wa Kitonga kumekuwa kunatokea ajali mara kwa mara hakuna crane ya kusaidia kuondoa magari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile wamekuwa mara nyingi kwenye Mto Ruaha watoto wetu wa shule wanazama, tunapata ajali, wananchi wanazama, hawana hata vifaa vya uokozi vya maji. Kwa hiyo ningeomba kwa kweli hili Jeshi la Zimamoto hebu liangaliwe, lipewe pesa ya kutosha ili wananchi waweze kuishi bila ya kuwa na matatizo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishauri halmashauri zetu tunapotenga haya maeneo basi tuweke na maeneo kwa ajili ya kuonesha huduma hii ya zimamoto kwa sababu tumeona sasa hivi miji inakua, lakini inapotokea ajali haya magari yanashindwa kupita kwenda kuokoa. Hata hapa Dodoma ilitokea siku ile walibomoa nyumba. Kwa hiyo, niombe Halmashauri zetu pia zitenge maeneo kuhakikisha kwamba magari ya zimamoto yanakwenda kufanya kazi zao vizuri. Vilevile naona magari yale ya washawasha yanatumika kuzima moto. Sasa naomba Jeshi letu la Zimamoto wapewe magari ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze Kamanda wa Jeshi la Magereza na hasa wa Mkoa wetu wa Iringa, Kamanda Mwakajungu anafanya kazi nzuri sana. Nilishakwenda kutembelea Magereza, chakula kizuri sana lakini wafungwa hawana uniform kwa kweli, wanavaa kwa shida. Iringa ni mji ambao una baridi sana, wapewe masweta na mablanketi, kwa kuwa unakuta wafungwa wanaugua pneumonia. Kwa hiyo, wanatumia pesa nyingi kuwatibu badala ya kuzuia na wanapata matatizo makubwa sana kwa kuhudumia hayo matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niendelee kuzungumzia kwamba Wilaya ya Kilolo ni Wilaya ya muda mrefu sana bado haijaweza kujengewa Ofisi ya Wilaya. OCD anakaa mbali na DC, kwanza hawana vifaa vya kutosha kwenye ile Wilaya, kwa sababu hawana mafuta, vilevile hawajawahi kujengewa nyumba za kuishi, siku zote wamekuwa wakiishi kwenye maeneo ye makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, askari amepanga kwa mwananchi, je, yule mwananchi akifanya kosa na yeye amepanga kwake kweli atam-report? Kwa hiyo, niombe kwa kweli Jeshi la Polisi liangalie, askari wote waishi kambini kwa sababu wakati mwingine wanakuwa hawana usafiri. Kwa mfano, Kilolo, Makao Makuu ya Polisi ambayo wamepewa yako mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee kuzungumza kuhusiana na maandamano. Kwa kweli nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuondoa haya maandamano, kwa sababu kwenye Mkoa wetu wa Iringa, maandamano haya yametuletea hasara kubwa sana, yalisababisha hata gari la zimamoto lilipigwa vibaya sana, lilivunjwa vunjwa kwa ajili ya maandamano. Vilevile barabara nyingi sana ziliweza kuchomwa wakati huo na kusababisha hasara sana kwenye Mkoa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gumu sana ambalo akinamama wote kwa kweli tumelipongeza kuhusu maandamano, watoto wengi sana walivunjwa miguu, waliumia sana na hawakuweza kupatiwa msaada wowote. Kwa hiyo, nasema kwamba wananchi waandamane kwa kufanya kazi, wasiandamane kwa kuharibu vitu na niwaombe hata wanasiasa wenzangu tufanye hawa watu waandamane kwa kufanya kazi, nafikiri itakuwa busara zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee kuhusiana na mtandao wa wanawake, maana yake sisi ni wanawake, nilikuwa mgeni rasmi kwenye shughuli ya sikukuu ya mtandao wa wanawake. Kwa kweli walionesha wanafanya kazi nzuri sana. Kila idara wapo lakini cha kushangaza IGP yuko hapa, ukitembea kule kote hawapati vile vitochi, vitochi hivi vinapewa kwa masharti, naona wanashika tu wanaume. Walikuwa wanasema kwamba hata wanawake wanaweza wakashika vile vitochi wakafanya kazi vizuri tu. Sijajua kwamba wanapewa kwa masharti vitochi ama walipewa kwa waganga wa kienyeji. Kwa hiyo, niombe hata wanawake pia wapewe vitochi siyo kwamba wanaume tu siku zote.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri Mheshimiwa Jafo kwa kazi nzuri sana ambayo amekuwa akiifanya. Pia niwapongeze Naibu Mawaziri Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege bila kumsahau Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu bila malipo, nimpongeze sana kwa sera yake ya elimu bila malipo kwa sababu imesaidia vijana wengi kupata nafasi ya kusoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie changamoto katika shule za msingi katika Mkoa wa Iringa. Ukarabati wa majengo na miundombinu, majengo ya shule za msingi yana hali mbaya sana sababu halmashauri nyingi zinaweka vipaumbele katika ujenzi wa sekondari na maabara kutokana na ufinyu wa bajeti zilizopo katika halmashauri.

Changamoto nyingine katika shule hizi ni malipo ya maji, umeme na walinzi na hii inasababisha hata vyoo kutotumika. Naomba Serikali kama ilivyotoa malipo kwa ajili ya elimu iondoe pia gharama za maji na umeme mashuleni, shule zina bills kubwa sana wanakatiwa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ucheleweshwaji wa fedha katika miradi ya maendeleo katika halmashauri. Serikali iangalie miradi yenye tija katika halmashauri zetu ili iweze kuleta pesa kwa wakati katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa machinjio ya kisasa Iringa Manispaa. Mradi huu ni wa muda mrefu sana, tulianza toka 2008 unahitaji sasa 1.4 bilioni. Ni chanzo kizuri sana, mapato katika halmashauri yetu na ukimalizika utaweza kutoa ajira kwa wananchi zaidi ya 200. Ni vyema tukae na miradi michache na tuwe na miradi ya vipaumbele kuliko kuwekeza pesa kidogo katika miradi mingi ambayo inachelewa kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA naipongeza Serikali kwa kuamisha huu wakala kwa ajili ya kushughulikia barabara za halmashauri ningeomba Serikali iiwezeshe TARURA kutengewa bajeti ya kutosha ofisi, wataalam na vifaa kama magari kwa sababu pamoja kazi kubwa waliyonayo bado wanapata shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Manispaa yetu ya Iringa kuna mradi wa Daraja la Tagamenda lipo Igumbilo. Daraja hili limechukua muda mrefu sana, kuna majanga huwa kila mwaka yanatokea maafa makubwa, vifo, sababu kuna shule ya sekondari na wananchi ambao wanategemea
kutumia daraja hilo. Sasa tumeambiwa daraja hilo limehamishiwa TARURA, ningependa kupatiwa majibu, tulipohoji katika manispaa yetu tuliambiwa Serikali imeleta fedha ya kutosha kumaliza daraja, hilo je, ni kweli na je, daraja hilo lini litakamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa mgao wa shilingi 4.5 bilioni zilizotengwa wa ajili ya hospitali zetu za Mkoa wa Iringa, Hospitali ya Kilolo, Mufindi na Iringa DC. Hospitali yetu Iringa Manispaa haijatengewa pesa yoyote na kuna changamoto kubwa sana ya jengo la vipimo, pia hakuna mashine za x-ray, T-scan, ultrasound, hakuna ward za kulaza wagonjwa wengine kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali ya mkoa. Pia tunamshukuru sana Waziri wetu, Mheshimiwa Jafo alipita na aliona hiyo changamoto. Naomba Serikali ilichukue hilo kwa uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Elimu Mheshimiwa Prof. Ndalichako na Naibu Waziri, Mheshimiwa Ole Nasha na Makatibu kwa hotuba yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali hii ya Awamu ya Tano ikiwemo ukarabati wa shule kongwe nchini. Ongezeko la mikopo elimu ya juu, ukarabati wa ujenzi wa vyuo nchini na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata ufafanuzi kwa mambo yafuatayo: ukarabati wa shule ya Lugalo Sekondari Mkoa wa Iringa. Shule hii inafundisha pia watoto wenye uhitaji maalum. Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha shule hii inapatiwa kipaumbele katika ukarabati wa miundombinu ikiwamo na ujenzi wa uzio kwa sababu wanafunzi wenye uhitaji maalum wanasoma kwa shida sana? Naipongeza Serikali kwa kupeleka vifaa kwa wanafunzi wenye uhitaji maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iangalie Sera ya Elimu ya kubadili mitaala mara kwa mara bila kuwapatia mafunzo walimu. Changamoto hii ni kubwa sana. Serikali inaweka mkakati gani wa kuhakikisha kabla ya kubadilisha mitaala waalimu wapatiwe mafunzo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wetu wengi wanafanya kazi nzuri katika mazingira magumu. Je, nini mkakati wa Serikali kutoa motisha kwa walimu wa shule zinazofanya vizuri kwenye matokeo ya Kitaifa? Ni vema zingeandaliwa tuzo maalum ili kuleta hamasa kwa shule na walimu wengi kufanya vizuri. Sambamba na hilo, walimu wamekuwa na changamoto kubwa sana ya upandishwaji wa madaraja kwa walimu walioajiriwa kuanzia mwaka 2012 - 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH);ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha inatenga pesa ya kutosha ili tafiti ziweze kufanyika? Kwa sababu maendeleo ya kisayansi na teknolojia ambayo ndiyo msingi wa maendeleo ya kiuchumi katika Taifa lolote lililoendelea tunategemea sana kiwango cha ugunduzi na ubunifu unaotokana na elimu bora inayotolewa. Vijana wetu wamekuwa na ubunifu mbalimbali, sijaelewa Serikali inawasaidiaje wabunifu au wagunduzi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mkurugenzi, ameweza kusimamia vizuri sana japo kuwa uangaliwe utaratibu wa kutoa mikopo watoto yatima waliokuwa wanasomeshwa na mfadhili, uwepo utaratibu wa kuwatambua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Mpango wa Taifa wa Serikali. Nianze kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, nimpongeze pia Waziri Mkuu wetu, nipongeze Mawaziri wote wa Serikali ya Awamu hii ya Tano kwa kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya kwa kipindi cha miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendele pia kumpongeza sana, kupongeza sana Wabunge wote ambao wamehamia CCM kutoka upinzani kwa kuona kazi nzuri sana inayofanywa na Mheshimiwa Rais, kwa kuona kazi nzuri sana inayofanywa na Mawaziri wetu na kuamua kuja CCM, kwa hiyo nikwambie Mheshimiwa Jenista jiandae kazi yako ni nzuri tutaendelea kujaa huku kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Mpango, kama jina lake lilivyo kwa mpango mzuri, Naibu wake, Dkt. Kijaji, watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri ambayo wametuletea huu mpango mzuri wa maendeleo ambao kwa kweli umepanga ukapangika, na ndio maana sasa hivi unatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee, mimi leo nikupongeza kwa sababu mambo mazuri yanaonekana, niendelee kumpongeza Rais wetu na Serikali yetu na Chama chetu cha Mapinduzi kwa miradi ambayo sasa hivi yameanza kutekelezeka ya kielelezo ujenzi wa reli ya kati, ujenzi wa barabara wa barabara ya juu (Mfugale fyover) ujenzi wa viwanja vya ndege, uboreshaji wa shirika la ndege, mradi wa kuzalisha umeme maji - Rufiji, mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda mpaka Tanga na miradi mingine mingi tu nikiitaja hapa muda utaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika ukurasa wa 32 wa kitabu cha hotuba ya Waziri Mpango, niendelee kupongeza marekebisho ya Sheria ya Madini, kwa kweli niendelee kuwapongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri kwa kufanya marekebisho ya Sheria za Madini zilizofanyiwa
mapitio ili kuwezesha Serikali yetu kunufaika zaidi na rasilimali za madini ambayo imewezesha ongezeko la mapato kwa kipindi cha mwaka 2017/2018 lengo ambalo lilikuwa limewekwa na Serikali kwa mrabaha na ada za mwaka za leseni ilikuwa shilingi bilioni 194; lakini imeweza kukusanya bilioni 301.2 ambayo sawasawa na asilimia 56, kwa kweli hilo ni jambo kubwa sana. Tutakumbuka kwamba jinsi sheria hii ilivyokuwa imeleta matatizo makubwa wenzetu walikuwa hawaielewi lakini sasa hivi Serikali imeweza kupata mapato makubwa sana kupitia marekebisho ya sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kupitia sheria hii imeweza kuweka katazo la kusafirisha madini ghafi ambayo hayajawekewa thamani. Ushauri wangu kwa Serikali, Serikali iweke mazingira wezeshi kwa kuondoa kodi katika mashine za ukataji wa madini ya vito. Hii itasaidia kuwa na wakataji wengi wa madini ya vito na pia itasaidia ajira kwa vijana wetu kupitia madini. Pia kuweka mazingira wezeshi ya kusaidia shughuli za wachimbaji wadogo wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe Serikali iweze kuwasaidia kuwawekea mazingira wakina mama ili waweze kujiajiri kupitia madini kama vile kuna Chama cha TAWOMA ambacho ni chama cha wachimbaji wanawake kote nchini pia kiwezeshwe ili sisi wakina mama pia tuweze kujiajiri kupitia madini. Pia nishauri kwamba wawepo Maafisa Madini wa Mkoa kuliko walivyo wa kanda ilivyo sasa hivi ili kusaidia hii sekta ya madini waweze kukusanya pesa katika mikoa yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukienda katika ukurasa wa 33 unaelezea kuhusu elimu. Niipongeze Serikali yetu kwa utaratibu wa kutoa elimu bila malipo katika shule zetu ambapo wameweza kutumia shilingi bilioni 20.9 kila mwezi. Ukifungamanisha uchumi na maendeleo ya watu, mpango wa kuendeleza ufaulu katika masomo ya hesabu na sayansi na kuendelea kutoa elimu inayozingatia mahitaji halisi ya soko la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, sasa naiomba Serikali iwe na mikakati ya kuhakikisha kwamba shule zetu nchini zinaboreshewe maabara kwa sababu maabara katika shule nyingi bado hazijakamilika, lakini pia walimu bado hawatoshelezi kuwepo katika shule kufundisha hii elimu ya sayansi, lakini pia na vifaa vya maabara Serikali ijitahidi kwa sababu sasa hivi tunatakiwa tuandae wanasayansi wengi sana ili kusaidia huu uchumi wa viwanda, vijana wetu waweze kuajiriwa na tuweze sisi wenyewe kuwa na vijana ambao wanatumikia viwanda vyao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba tu nitoe mfano wa nchi ya Singapore; unaona nchi ya Singapore ilikuwa ni nchi ambayo ina uchumi duni sana, lakini kuna yule Waziri Mkuu ambaye ni kiongozi wao anaitwa Lee Kuan Yew yeye kwakweli kwanza kabisa alivyoanza kuinua uchumi wa Singapore walimuona kama dikteta lakini sasa hivi alipofariki wamemkumbuka kwa sababu uchumi wa Singapore sasa hivi umekuwa upo juu sana na unaona yeye aliamua kutoa elimu kwa vijana wake wa Singapore na sasa hivi vijana wameweza kujiajiri, kuajiriwa na kutengeneza uchumi kwa kutumia viwanda walivyonavyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, asante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie hoja hizi za Wenyeviti watatu. Kwanza kabisa, nianze kuwapongeza Wenyeviti wote wa Kamati tatu ambazo wamewasilisha taarifa zao hapa Bungeni. Pia nitoe pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais wetu John Pombe Magufuli na kwa Mawaziri wote ambao Wizara zao ziko kwenye hizi Kamati kwa kazi nzuri sana ambazo wamekuwa wakizifanya na kwa kweli wanaitendea haki nchi yetu na Chama chetu cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba niipongeze Serikali kwa utoaji wa pesa kwa ajili ya Hospitali za Wilaya 67. Kwa kweli pesa hizi hata katika Mkoa wetu tumepata Iringa DC, Kilolo na Mufindi lakini naomba nitoe ombi maalum. Katika Mkoa wetu wa Iringa tunayo hospitali ambayo ipo katika Manispaa yetu, Hospitali ya Frelimo, Iringa Mjini ambayo iliazishwa mwaka 2013, naomba Serikali yetu iwapatie pesa kwa sababu kabla ya hizi pesa hazijaenda kujenga hospitali za wilaya hizi nilizozitaja wagonjwa wanatibiwa katika hospitali hii. Kwa hiyo, naomba Serikali ingeangalia kama kuna uwezekano wa kuhakikisha kwamba hizi hospitali ambazo zinafanya kazi basi zipewe kipaumbele. Hii hospitali ingejengewa wodi za akina mama, akina baba na watoto ingeweza kusaidia hata kupunguza msongamano mkubwa ambao upo katika hospitali yetu ya mkoa. Vilevile ingeweza kujengewa hata jengo la vipimo ambalo kwa kweli imekuwa ni tatizo. Kwa hiyo, niombe ombi maalum kwamba sasa hivi tumalizie hizi hospitali ambazo zipo na tayari zimeanza kusaidia maana hospitali hii imesaidia kupunguza vifo vya akina mama na watoto katika Mkoa wetu wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna changamoto kubwa sana katika Hospitali ya Mkoa, kuna mwingiliano katika Hospitali ya Mkoa na katika Gereza la Mkoa. Mwingiliano huo kwa kweli ni mkubwa sana kwa sababu kuna wakati ambapo barabara zinafungwa, wagonjwa wanashindwa kupelekwa hospitali wakati wanapeleka wafungwa kwenye gereza. Kwa hiyo, naomba kipaumbele kitolewe kwa sababu bale wanashindwa hata kuongeza majengo kwa ajili ya Hospitali yetu ya Mkoa ambayo Serikali yetu sasa hivi imesema hizi hospitali za Mikoa zitakuwa za rufaa na zingeweza kusaidia sana katika Mkoa wetu wa Iringa na Nyanda za Juu kwa suala zima la matibabu. Katika Hospitali ya Mkoa hakuna nyumba za Madaktari Bigwa, kwa hiyo, wananchi wanapata shida sana, hili ni ombi maalum.

Mheshimiwa Spika, nimwombe tu kaka yetu Mheshimiwa Sugu kwenye Wizara ya Afya kazi kubwa imefanyika. Kuna vingine ambavyo Wapinzani mnatakiwa muunge mkono. Nishukuru safari hii mengi mnayaunga mkono na iwe hivyo kwa sababu ni kwa nia nzuri kabisa Serikali yetu inafanya kazi hizo. Nimpongeze Mheshimiwa Tulia anafanya kazi nzuri sana, amewatendea haki sana wananchi wa Mbeya, kwa kweli hongera zako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda ukurasa wa 37 na 38 wa Kamati ya Huduma za Jamii, naomba niunge mkono kabisa ushauri wa Kamati hii wa kuiwezesha Idara ya Maendeleo ya Jamii. Idara hii mara nyingi imekuwa haipatiwi pesa za kutosha na ndiyo ambayo inasaidia jamii na sasa hivi tuna tatizo kubwa sana la watoto kubakwa na vifo vya watoto.

Mheshimiwa Spika, vilevile, napenda kujua Benki yetu ya Wanawake imefikia wa wapi, kwa sababu najua idara hii ipo chini yake. Kuna wakati kulikuwa na sintofahamu kwamba na yenyewe imetangazwa na Benki Kuu hata akina mama sasa wameingia wasiwasi kwamba hii benki sasa inawasaidiaje wanawake? Benki hii tulikuwa tunajua ndiyo suluhisho la akina mama kwamba hatupati zile shida za benki nyingine ambazo zimekuwa zikituzalilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nielezee pia kuhusu bima ya afya. Niombe katika bima ya afya kuna ile package ya Sh.1,500,000 ambapo huduma anapata baba, mama na watoto wanne lakini utakuta kina mama wengi au familia sasa hivi ile package hawasaidii kwa sababu watoto wakiwa juu ya miaka 18 hawatibiwi. Nashauri ingekuwa vizuri ikawepo na package ya mtu mmoja pengine iwe Sh.500,000 ili kama watoto wangu wameshafikisha miaka 18 niweze kumkatia bima yake ama kama nina mzazi wangu basi niweze kumkatia bima yake au mama mwingine ni mjane, wababa wengine ni wagane inakuwa haina maana kuchukua package nzima. Kwa hiyo, naomba suala hili lingeangaliwa ili kuweza kusaidia wananchi ambao wanahitaji bima kwa ile package ya juu kwa maana ya grade one. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuchangia kuhusu ukarabati wa shule zetu za msingi. Kwa kweli hili ni tatizo kubwa sana. Katika Mkoa wetu wa Iringa shule nyingi sana za msingi ni za siku nyingi sana. Kwanza nipongeze Serikali kwa ukarabati shule kongwe za sekondari, Ifunda imetuhusu, shule nyingi kweli zimekarabatiwa, kwa kweli nipongeze.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe hizi shule za msingi kwa sababu katika halmashauri zetu bado hakuna uwezo wa kuzikarabati. Mara nyingi tumekuwa tukianza kujenga madarasa kwa ajili ya hii elimu bure, kwanza nimpongeze Rais kwa elimu bure katika Mkoa wa Iringa, lakini kuna tatizo ambalo limejitokeza kutokana na ukongwe wa hizi shule za msingi basi vyoo ndiyo haviingiliki kabisa. Watoto wetu sasa wamepata hata tatizo la kubakwa sababu mojawapo ni kwamba wanakwenda kuomba kujisaidia kwenye vyoo vya jirani na shule hazina uzio. Kwa hiyo, naomba Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi iangalie kabisa hizi shule za msing kwa sababu ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee kuhusu capitation fund. Wanapotoa hii fund wanaangalia idadi ya watoto lakini hawaagalii matatizo yaliyopo. Kwa mfano, sasa hivi shule nyingi sana wanashindwa kulipia maji, umeme na zile gharama ndogo ndogo. Kwa hiyo, kuna zile shule ambazo idadi ya watoto siyo wengi lakini wanatakiwa kugharamia huduma hizo nilizosisema, nashauri labda wangeangalia jinsi ya kuwa na mfumo mwingine.

Mheshimiwa Spika, utakuta shule zetu hizi za msingi wamekatiwa maji hivyo watoto wanapata shida sana. Kwa sababu sasa hivi ni elimu bure pengine tungewaacha watoto wasikatiwe maji kwani wamekuwa wakipata matatizo sana mfano kunapokuwa na magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu. Kwa kweli shule nyingi za msingi hata za sekondari hazina maji labda tungeangalia mfumo mwingine mzuri wa kusaidia shule hizo ili wasikatiwe maji bali shule iendelee kudaiwa au Serikali iangalie njia nzuri zaidi ya kusaidia hizi shule zetu za msingi ili kuondokana na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nielezee kuhusiana na timu zetu ambazo zinazocheza daraja la kwanza hasa za wanawake. Kwa mfano, pale Iringa kuna timu ya Panama inashiriki hili kombe kwenye mazingira magumu sana. Nafikiri nilishamwambia hata Waziri tuone tunawasaidiaje hawa watoto wa kike na pale kuna vipaji vikubwa sana lakini utakuta wanashindwa kwenda kushiriki sehemu nyingine au wanakwenda kwa shida au wanatembeza mabakuli kiasi kwamba hawa watoto wakike wanaweza kupata masharti mengine. Naomba Wizara ya Michezo ingalie njia nzuri ya kusaidia hizi timu za wanawake ambao wanashiriki ligi kuu ya daraja la kwanza kwa sababu najua pale ndiyo tutapata vipaji vya kuunda timu ya Taifa kutoka kwenye mikoa mingine. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie katika Wizara ya Mambo ya Ndani. Namtanguliza Mwenyezi Mungu katika mchango wangu, lakini nami niungane na mchangiaji aliyepita kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwachagua hawa Mawaziri na viongozi wote waliopo katika Jeshi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Kangi Lugola; Naibu Waziri, Mheshimiwa Masauni; Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hii ya Mambo ya Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze makamanda wote kwa kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya, IGP Sirro, SGP Kasike, Zimamoto, SGP Andengenye na Uhamiaji SGI AP Dkt. Makakala ambaye kwa kweli ni mwanamke aliyetuwakilisha wanawake wote na amefanya kazi nzuri sana. Katika ripoti ya Mheshimiwa Waziri tumeona amepewa tuzo katika passport. Kwa hiyo, tunaona kwamba sisi wanawake tumewakilishwa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kazi nzuri ya mama huyu, nafikiri hata mtandao wa Polisi, sasa uangalie wanawake na wenyewe wale wanaoweza, basi wapatiwe vyeo vya juu ili waendelee kutuwakilisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Askari wetu wanafanya kazi nzuri sana lakini tukikutana na bajeti finyu wamekuwa wakifanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali iwaangalie, kuna changamoto ambazo wanakumbana nazo. Wanadai posho zao muda mrefu, uhaba wa watumishi, pensheni zao zilipwe kwa wakati, promotion zao wapatiwe kwa wakati ili kuwatendea haki na wawe na ari ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais pia kwa kuona changamoto zilizopo katika nyumba za Maaskari wetu, naona ameanza kuzifanyia kazi pale Ukonga. Nami namwomba katika Mkoa wetu wa Iringa Askari wetu wanakaa katika nyumba chakavu sana. Ukiangalia pale Iringa Mjini, Mufindi, kule Kilolo ndiyo hakuna kabisa nyumba za Askari Polisi na wengine wanakaa nje ya makambi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iangalie. Pamoja na uchakavu walionao, kuna akina mama kuna watoto ambao wamekuwa wakiishi kwenye mazingira magumu sana. Kwa hiyo, tunapozungumzia makazi ya Polisi, tunaangalia hata akina mama na watoto walioko katika nyumba zile. Kwa hiyo, naomba hili lizingatiwe kwa umuhimu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ya Kilolo, toka ianzishwe Makao Makuu ya Wilaya, OCD hajawahi kujengewa Ofisi katika Makao Makuu ya Wilaya. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto kubwa sana. Tunawashukuru sana TAZAMA Pipeline ambao wamempatia ofisi, lakini ni mbali sana na ilipo Mahakama. Kwa hiyo, utakuta wakati mwingine wanapata shida sana kuwapeleka mahabusu kwenda kwenye Mahakama kwa sababu ni karibu kilomita 70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba waangalie, kuna gharama kubwa kila siku zinatumika. Wangeangaliwa changamoto iliyopo katika Wilaya ya Kilolo ili Mahakama ijengwe yalipo Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nikizungumzia Jeshi la Zimamoto wana changamoto nyingi sana na wanafanya kazi vizuri sana katika mkoa wetu lakini pia posho zao wanakuwa hawalipwi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uhaba wa magari ya Zimamoto. Utaona katika Wilaya ya Mufindi kuna msitu ambapo mara nyingi moto umekuwa ukitokea lakini hakuna gari la Zimamoto. Vilevile Wilaya ya Kilolo hakuna gari la Zimamoto na mara nyingine kumekuwa kukitokea ajali nyingi katika mlima Kitonga na hakuna hata gari la uokozi (crane) kwa ajili ya kusaidia kunapotokea ajali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu mkubwa wa Askari katika Wilaya zote. Jeshi la Magereza vilevile kuna madeni ya posho, kuna madeni ya Wazabuni ambao wamekuwa wakisaidia kuwalisha wale wafungwa, gharama za kuwasafirisha mahabusu na wafungwa wanaostahili kwenda kusikiliza kesi zao pia ni tatizo. Kwa hiyo, naomba Serikali ingeangalia pia haya Majeshi ili wapatiwe fungu la kutosha katika Mkoa wetu wa Iringa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu sasa. Naomba nitoe ushauri kwa Serikali kuhusiana na Jeshi la Zimamoto. Zile pesa za makusanyo (fire inspection fee) kwenye nyumba, biashara, viwanda, ma-guest, migodi, pengine ingekuwa hata asilimia kumi zinaenda kununua hivi vifaa vya Zimamoto ingeweza kusaidia upungufu ambao upo katika hili Jeshi la Zimamoto kuliko ambavyo sasa hivi pesa zote zinachukuliwa na Serikali wakati wao wenyewe wanakuwa wana matatizo kabisa ya upungufu wa vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Jeshi la Magereza, Magereza iwe kama Chuo cha Mafunzo, waongezewe vifaa vya mafunzo ili wale wafungwa waliopo kule wawe wanapatiwa mafunzo. Vilevile wapewe vifaa vya kilimo kama matrekta, yatasaidia; na waweze kufundishwa hata uvuvi na wapatiwe mkopo usiokuwa na riba ili waweze kujiendesha wenyewe. Kwa hiyo, itasaidia.

Mheshimiwa Mweyekiti, nimeona hata Mheshimiwa Rais anasema kwamba haya Magereza yangekuwa yanajiendesha yenyewe katika kulisha wafungwa na kusaidia changamoto zilizopo. Kwa hiyo, kama tukiziwezesha kupata mikopo, inaweza ikasaidia sana zikawa zinajiendesha zenyewe; na wapewe kazi za ujenzi. Kwa hiyo, utaona kwamba tutakuwa tumezisaidia, tutakuwa hatutumii tena ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kutoa mfano, nimeshatembelea pale Magereza nikakuta wana kiwanda, lakini wana changamoto ya fedha. Namshukuru Mkurugenzi aliweza kuwakopesha shilingi milioni kumi na sasa hivi wanajiendesha tu vizuri katika gereza letu la Mkoa wa Iringa. Kwa hiyo, iwe mfano hata katika Magereza nyingine, bado tunaweza tukaziwezesha Magereza zikaweza zikajiendesha zenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lingine, Mkoa wetu una changamoto ambao kuna mwingiliano mkubwa sana kati ya Gereza la Mkoa na Hospitali ya Mkoa. Hili nimekuwa nikilizungumzia mara nyingi sana; na ningeomba labda sasa hivi hebu mlipe kipaumbele kwamba kwa sababu Gereza lina eneo kubwa nje ya mkoa, basi lihame ili kupisha hospitali iweze kujenga majengo na nyumba za Madaktari iweze kusaidia wagonjwa wetu na msongamano uliopo katika Hospitali ya Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Jeshi la Magereza liwe linawapatia hati maalum wadau wanaosaidia Jeshi la Polisi. Kwa mfano, katika mkoa wetu kuna wadau ambao wameweza kusaidia sana ujenzi wa Vituo vya Polisi, ujenzi wa madawati, wamekuwa wakisaidia hata ukarabati wa majengo mbalimbali, kwa mfano, yuko huyu Mheshimiwa ASAS ambaye ni mmiliki wetu pale Mkoa wa Iringa, kuna Besania, kuna Mbarak kuna Ruaha National Park, Zakharia Hanspop ambaye pia kwa kweli ametupatia magari ya Zimamoto na Ambulance. Sasa uwepo utaratibu mzuri wa kuwapatia hati ambayo inatambulika kwamba wamesaidia Jeshi letu la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi mwenyewe nilijenga Kituo cha Polisi pale Kihesa, pia ni vizuri nikatambulika mchango wangu kwa kupatiwa hati maalum kwa sababu nimelisaidia Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nizungumzie kuhusiana na vitambulisho vya Taifa. Hivi vitambulisho nafikiri Wabunge walio wengi pia wamezungumzia kwamba wengi walishakwenda kupiga picha, wamefanyiwa kila kitu, lakini sasa vitambulisho bado havijawafikia; na mara nyingi sasa hivi kila sehemu unatakiwa uwe na hicho kitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna ufinyu wa bajeti, basi Serikali iangalie uwezekano wa kutoa pesa ya kutosha ili kuhakikisha kwamba hivi vitambulisho wananchi wanapewa haki yao, kwa sababu kila unapotaka kwenda lazima uwe na kitambulisho. Hata ukisafiri nchi za nje lazima uwe na kitambulisho cha Taifa. Vilevile ukitaka labda kuomba passport lazima uwe na kitambulisho. Kwa hiyo, wananchi wamekuwa wakipata shida sana wanapotakiwa kupata hivi vitambulisho.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante. Muda wetu ndiyo huo.

MHE. RITTA E. KABATI: Naomba niunge mkono hoja hii. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Waziri Mheshimiwa Eng. Kamwelwe, Manaibu Mawaziri Mheshimiwa Kwandikwa, Mheshimiwa Eng. Nditiye, Makatibu Wakuu na Watendaji wa taasisi zote kwa kazi nzuri sana zilizofanywa na kwa kuwasilisha hotuba hii ya bajeti.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuhusu ujenzi wa viwanja vya ndege. Naishukuru sana Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa ahadi ya ujenzi wa viwanja kikiwepo kiwanja cha Nduli Iringa. Nilikuwa naomba Serikali ijitahidi pia kutoa fidia kwa wakati kwa wananchi walioguswa na upanuzi wa kiwanja hicho.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuhusu Shirika la Ndege ATCL. Niungane na wote walioipongeza Serikali kwa ununuzi wa ndege sita. Napongeza pia kwa kuanzisha mfuko wa ndege katika kiwanja chetu cha Iringa, tunaamini sasa hata uchumi wetu kupitia utalii utaongezeka.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iangalie uwezekano wa kuwa na connection ya kiwanja cha Dodoma angalau kuwa na miruko mfano Mwanza – Dodoma, Mbeya – Iringa, Dodoma – Songea, Dodoma – Dar es Salaam ili kuwe na urahisi wa Makao Makuu kufikika kwa urahisi na abiria ni wengi. Vilevile bei za nauli za ndege ziangaliwe ili abiria wapande wengi.

Mheshimiwa Spika, Sekta hii ya Ujenzi inafanya kazi nzuri sana hapa nchini. Napongeza sana kazi nzuri ya ujenzi wa barabara nchini ikiwepo na mkoa wetu wa Iringa. Katika Mkoa wa Iringa naomba Serikali iangalie na kujenga barabara ya mchepuo itakayosaidia kuchepusha magari makubwa sana kupitia katikati ya mji.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya magari makubwa kupita katikati ya mji, kwanza yanaweza kusababisha ajali na hatari kubwa mno. Barabara ni finyu na kuna maduka hoteli na biashara ambazo zinafanya wananchi kuegesha magari na vyombo vya moto katika barabara hiyo. Pia changamoto ni kwamba wafanyabiashara wanashindwa kufanya biashara. Ni lini sasa barabara hiyo ya mchepuo itajengwa ili kuchepusha hayo magari kupita katikati ya Mji wa Iringa?

Mheshimiwa Spika, barabara ya Dodoma – Iringa, ukipita katika kona za Nyangoro, kuna maporomoko ya mawe na wakati wa mvua yanaongezeka. Nimeshauliza sana maswali kuhusiana na changamoto hiyo: Je, ni mkakati gani unawekwa ili kuondoa changamoto hiyo?

Mheshimiwa Spika, lingine ni ujenzi wa reli. Naipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa inayofanywa ya kwa ujenzi wa reli hiyo. Ukikamilika utasaidia hata uharibifu wa barabara zetu ambazo zinaharibika kwa kubeba mizigo mizito. Ujenzi huo mpaka sasa umefikia asilimia 50 phase one Dar es Salaam – Morogoro. Mradi huu ukikamilika, utaleta ajira 10,000,000. Ni kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza kwa maboresho makubwa mbalimbali ya sheria na elimu kwa bodaboda na bajaji. Pongezi kwa mtambo wa VTS, umesaidia kupunguza ajali barabarani. Changamoto kubwa ni abiria, wakipata ajali wanapata taabu sana. Ni lini Serikali italeta sheria ya kuweka miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu?

Mheshimiwa Spika, TTCL wanafanya kazi nzuri sana. Je, yale madeni wanayodai katika taasisi za Serikali watalipwa kwa utaratibu gani?

Mheshimiwa Spika, UCSAF inafanya kazi nzuri sana, maeneo mengi yameweza kupata mawasiliano, lakini kuna maeneo bado hayajapata mawasiliano. Kwa mfano, Mafinga ni Kata ya Ideta, Ihowanza – Ipimo – Ihowasa – Kilolo – Kata ya Ihimbo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziro Mpina, Naibu Waziri Mheshimiwa Ulega, Makatibu Wakuu na Watendaji wa Wizara ya Mifugo kwa hotuba yao nzuri ya bajeti iliyowasirishwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, naomba na mimi nitoe mchango wangu kwa mambo yafuatayo;

Mheshimiwa Spika, Makusanyo ya Maduhuli. Niipongeze Wizara kwa juhudi kubwa sana ya ukusanyaji maduhuli ya zaidi ya asilimia 183. Hii imeonesha jinsi mlivyo makini sana. Yapo malalamiko kwa baadhi ya wavuvi ambao wamekuwa wakilalamikia watendaji wa Wizara kuwatoza faini kama kuna kosa lakini risiti wanayopatiwa inaandikwa kiwango kidogo cha fedha. Je, Serikali inatambua hilo? na je, hatua gani zinachukuliwa kwa watendaji kama hawa wanaoiibia Serikali na kuwanyanyasa wafugaji na wavuvi?

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya Halmashauri watendaji wa Serikali wamekuwa wakiwanyanyasa wafugaji. Je, Wizara imejipangaje kuona utaratibu wa sheria na kanuni zinafuatwa kumlinda mfugaji?

Mheshimiwa Spika, Maeneo ya Malisho na Migogoro ya Wafugaji. Serikali inaweka mkakati gani wa kuhakikisha inamaliza mgongano wa wafugaji baina ya wakulima na dhidi ya hifadhi za taifa kutokana na upungufu wa maeneo ya malisho?

Mheshimiwa Spika, wafugaji wamekuwa wakinyang’anywa mifugo yao na askari wa wanyamapori na kusababisha unyanyasaji mkubwa sana na wananchi kufilisiwa. Je, huwa wanatumia sheria gani?

Mheshimiwa Spika, Kuimarisha Sekta ya Maziwa. Serikali imejipangaje kusaidia viwanda vya maziwa nchini kwa kuondoa tozo nyingi? (ukurasa wa 28) kulinda viwanda vyetu na kuvutia wawekezaji wa nje na ndani ikiwa ni pamoja na kuongeza ajira nchini.

Mheshimiwa Spika, pia changamoto nyingine ni wingi wa taasisi za kudhibiti na ukaguzi zipatazo 11 ikiwa ni pamoja na kutoza kila flavor katika maziwa.

Mheshimiwa Spika, ningeomba Serikali itupatie mkakati wa kukuza sekta hii ya maziwa. Naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na pia nimshukuru Mwenyezi Mungu. Kwanza nianze na kumpongeza sana Dkt. Mpango kwa kuleta Mpango mzuri. Nimpongeze pia Dkt. Kijaji, nipongeze Makatibu na watendaji wote wa Wizara hii ambao wametuletea Mpango wetu na kutuwasilishia hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye kwa kweli ameweza kutekeleza mambo mengi sana ikiwepo miradi ya ujenzi wa reli ya kati, mradi wa kufufua umeme, kuimarisha ndege, ujenzi wa meli, ujenzi wa jengo la abiria na miradi mingi tu ambayo kwa kweli hii inaonesha ni jinsi gani Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyotekelezeka. Sioni ajabu kuona kwamba watu wengine wameweza kuacha kuchukua fomu au wamejitoa katika chaguzi kwa sababu, miradi mingi sana imeonesha jinsi gani ambavyo tumekuwa makini Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kutoa pongezi kwa mpango huu mzuri ambao umewasilishwa. Na hii ni pamoja na kuongeza ukusanyaji wa mapato, kudhibiti matumizi mabaya ya fedha, kuweka nidhamu kwa watumishi, kwa kweli haya ni mambo ambayo yamesababisha Serikali yetu kuweza kuendelea kufanya vizuri na kuendeleza miradi mingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze sasa kuchangia mpango wangu, naomba nijikite katika urahisi wa kufanya biashara, easy of doing busuness. Niipongeze Serikali kwa kuanza kuweka usajili katika mitandao, kwa kweli hii ni kazi nzuri na inafanywa kwa urahisi, lakini wako wafanyabisahara wengi wadogowadogo ambao sasa hawawezi kutumia mtandao ambao ni akinamama, vijana; sasa nione tu Serikali inaweka mpango gani kuhakikisha wanawafikia hawa wafanyabiashara wadogowadogo ili na wao wasajili biashara zao. Maana pengine kumekuwa na urasimu mkubwa sana wa kusajili hizi biashara kama hawana mtandao, sasa Serikali imejipangaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wekeni mpango mzuri kuhakikisha kwamba, tunapata wafanyabiashara wengi ambao wanasajili biashara ili tuweze kupata mapato na tuongeze pato katika huu mpango ambao mmetuletea. Na ikiwezekana kuwepo na stop centre ili watu hawa wasiwe wanasumbuliwa pengine wanaenda kwa afisa biashara, anaenda TRA, BRELA, OSHA, nini, sasa tuweke sehemu moja then baadaye Serikali iweze kutengeneza mkakati wa kuhakikisha wanagawana hayo mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na mpango wetu. Pia naomba ujikite kuona umuhimu wa kutenga pesa ya utafiti kwa sababu, katika miradi mingi sana tumeona yaani tumetembelea kwenye vituo vingi vya utafiti na tuna watafiti wazuri sana katika sekta nyingi hazifanyi vizuri kwa sababu bado hatujaweka mkakati kuhakikisha tunatumia zile tafiti au watafiti wetu, ili sekta zetu zifanye vizuri. Sasa nilikuwa naomba Serikali iangalie umuhimu wa kutenga lile pato ile asilimia moja, ili ziende kenye utafiti kwa sababu tumeona nchi nyingi zilizoendelea na zinafanya vizuri katika miradi yake wameweka kipaumbele katika tafiti. Sasa nina imani tukiweka tafiti zetu bado tutafanya vizuri sana na tutakusanya mapato mengi katika sekta zote katika Wizara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nilikuwa naomba mpango wetu pia ujikite katika kuwekeza zaidi katika vyuo vyetu hivi vya VETA. Tukiwekeza katika vyuo vya VETA tutapata wataalam wa kuweza kuendesha viwanda vyetu vidogovidogo, tutapata mafundi mchundo na tuweze kuwawezesha vijana kuanzisha viwanda vidogovidogo na akinamama kwa sababu, tukiwa na viwanda vidogovidogo tukichukulia katika nchi kwa mfano India, China, unaona viwanda vidogovidogo ni vingi sana kwa hiyo, tukiwa na viwanda vidogovidogo tutapata uchumi mkubwa. Kwa hiyo, kama tukisaidia hawa vijana wakapata ujuzi na kuanzisha hivi viwanda vidogovidogo basi tutasaidia Serikali yetu kuwa na mpango mzuri wa kupata pesa na kukusanya pesa ili sasa tuelekee kwenye huo uchumi wa viwanda ambao ndio tumejikitanao kwamba, sasa hivi tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile nilikuwa naomba kuna pesa huwa inakatwa SDL asilimia nne kutoka kwenye viwanda. Ni kwa nini sasa hii pesa angalo kidogo isipelekwe SIDO, ili SIDO waweze kuwakopesha vijana wetu waweze kufungua biashara wakipata yale mafunzo; hii nilikuwa natoa tu kama wazo langu kwamba, kwa Serikali ile SDL ya asilimia nne kutoka katika viwanda basi ipelekwe pia SIDO iweze kuwasaidia wanaoanzisha viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikuwa naomba mpango wetu ujikite katika ujenzi wa barabara za kiuchumi zilizopo katika mikoa yetu. Ikiwezekana zijengwe kwa kiwango cha lami ili ziweze kupitika muda wote kwa sababu nikichukulia mfano tu katika Mkoa wangu wa Iringa unakuta barabara nyingi sana za kiuchumi hazipitiki kwa muda wote. Wakati wa mvua kunakuwa barabara hazipitiki kwa hiyo, unaona kwamba, kwa mfano labda ukienda kule Mufindi malori yanakwama hata wiki nzima, Kilolo malori yanakwama, lakini pia tunao uchumi mwingine kwa mfano tukiimarisha uchumi katika Mbuga yetu ile ya Ruaha National Park nafikiri tunaweza tukapata ongezeko kubwa la watalii na tukaongeza pato la Taifa na pato la mkoa pia. Lakini ikiwepo na kuongezea TARURA pesa kwa sababu TARURA ndio sasa hivi wana kazi kubwa kuhakikisha kwamba, barabara za vijijini zinapitika muda wote na zinajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee katika mpango wetu. Katika miradi ya kimkakati nilikuwa naomba kwamba, miradi hii ya kimkakati ya kuongeza tija na mapato sasa tijikite kuwasaidia wakulima, wafugaji, wavuvi kwasababu, hii miradi ya kimkakati katika kila halmashauri ipo, sasa iangaliwe. Kama kuna halmashauri ambayo ina wakulima wengi basi ile miradi ya kimkakati ijikite katika kuwasaidia wakulima. Kama kuna wavuvi halmashauri basi ijikite kuhakikisha kwamba, wavuvi au wafugaji wanasaidiwa ili kusaidia pato katika halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa tu mfano kwenye sekta ya uvuvi unaona mapato yamepanda kutoka bilioni 21 mpaka bilioni 72 kwa hiyo, hapo kuna ongezeko kama la bilioni 51 na mapato ya samaki nje ya nchi bilioni 379 mpaka bilioni 691 na bado sasa hapa hawajaweza kuwezeshwa vizuri. Niko katika Kamati ya Kilimo, tunatembelea wavuvi wana changamoto nyingi sana, kama tukijikita kuwasaidia hawa wavuvi wakafanya vizuri sana tutatengeneza mapto mengi ambayo yatasaidia nchi hii na tutaweza kuweza kusaidia mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo niseme kwanza vilevile niipongeze Serikali kwa kuweza kutoa pesa katika halmashauri zetu kwa ajili ya kuwakopesha akinamama, vijana na watu wenye ulemavu, lakini niombe hizi pesa wanavyopewa bila kupata elimu bado hatujawasaidia. Kwa sababu, hizi pesa unapowakopesha unakopesha zirudi na wengine wakope, lakini tuna imani wafanye vizuri zaidi wawe na biashara kubwa ambapo katika biashara zao tutasaidia sasa kuleta pato, walipe kodi kwa wingi ili tuweze kusaidia nchi yetu kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo ni kuwashukuru sana. Namuomba Mwenyezi Mungu aendelee kusaidia Tanzania na amsaidie Mheshimiwa Dkt. Magufuli, ili mwakani wanaosusa wasuse tuendelee kufanya vizuri zaidi, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Kamati ya PAC na LAAC. Nianze kwanza kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo kwa kweli imefanya kazi kubwa sana. Vilevile nizipongeze Kamati ya PAC na LAAC kwa ripoti zao ambazo wameziwasilisha hapa. Tulipokuwa tunachangia zamani tulikuwa tunasema halmashauri zetu zilikuwa kama vichaka vile vya pesa nyingi tulikuwa tunazipeleka kwenye halmashauri, lakini tunaona miradi haikamiliki, lakini sasa hivi Serikali imefanya kazi kubwa sana ya kusimamia mapato katika halmashauri zetu na tunaona sasa miradi mingi sana inakamilika kwa wakati na mambo yanakwenda sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna machache ambayo nataka kuchangia; jambo la kwanza ni kuhusiana na mkopo, ile asilimia kumi, yaani asilimia nne akinamama, asilimia nne ya vijana na asilimia mbili ya watu wenye ulemavu. Kwanza niipongeze sana Serikali nimeona hata katika ripoti Kamati imesema kwamba ni kitu ambacho ilifanya kazi ikahakikisha kwamba inakuwa Sheria. Kwa hiyo hii ni pongezi pia kwa Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mchango wangu ni kwamba, nikitoa mfano kwenye halmashauri yangu, imefanya vizuri sana. Kwa mfano halmashauri yetu ina vikundi karibu 1200 na utaona kwa mwaka tukichukua 2018/2019, vikundi 98 viliweza kupatiwqa mikopo karibu milioni 400. Sasa ushauri wangu halmshauri nyingi sana hazina uwezo wa kukopesha, yaani hii pesa tulikuwa tuna imani kwamba akinamama, vijana na watu wenye ulemavu iweze kuwasaidia katika miradi ili waweze pia hata kuchangia kodi Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu ni kwamba, kuwepo na vikundi kwa mfano kuna makundi mengine yanafanya kazi nzuri sana, mtaji wao ni mkubwa wanapewa pesa kidogo inakuwa haiwasaidii, lakini kingekuwepo kiwango ambacho vile vikundi vikubwa viki- graduate wasikopeshwe na halmashauri, pengine kungekuwepo na Mfuko wa Vijana au Mfuko wa Rais, wale sasa wafanyabiashara wakubwa wakubwa wakopeshwe huko ili hawa wadogo waweze kukopeshwa na halmashauri ili na wenyewe waweze kupata ile pesa, vikundi vyao viweze kupata na kuendelea kuliko ilivyo sasa hivi ambapo pesa inakuwa haitoshi wanapewa kidogo kidogo kiasi kwamba inakuwa haiwasaidii wale vijana na akinamama.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo nilikuwa nataka kuchangia ni kuhusu madai ya wastaafu; kwa kweli wastaafu maana yake ni wafanyakazi ambao wameitumikia hii Serikali yetu kwa muda mrefu. Kuna walimu, kuna wauguzi, kuna wafanyakazi wengi ambao wamefanya lakini wanapostaafu wanacheleweshewa sana malipo yao. Wanakuwa na madeni makubwa sana. Mstaafu anastaafu anaanza kufuatilia lile fao mpaka anaweza akafa, anaweza akaugua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoa tu mfano kwenye Halmashauri yetu, unakuta Mwaka 2018/2019 na 2019/2020 wastaafu wanadai fedha kama milioni 81 sasa ukija Mwaka 2020/2021 wale ambao wanastaafu wanahitaji malipo ya karibu milioni 45. Sasa Serikali imeweka mpango mzuri sana, wafanyakazi wote wapo kwenye data wanajua kwamba Mwaka kesho watastaafu. Ni kwanini wasingekuwa wanawaandalia kabisa hawa ambao watategemea kustaafu kipindi kingine ili baadaye kusiwepo na usumbufu ambao wanaupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba kwa kweli Serikali ingefanya kitu kama hicho ili wastaafu wetu wengine wanakuwa wakishastaafu wanataka kwenda kwao lakini naona hizi pesa wanazodai ni kusafirisha mizigo kurudi kwao. Wastaafu wengine walikuwa ndiyo wanataka wakimaliza anagalau sasa waweze kusihi maisha mazuri lakini matokeo yake sasa wanaugua, wanakuwa wanapata mateso makubwa. Naomba Serikali, wanaostaafu mwakani leo hii iwawekee kabisa unapondoka wapewe cheque zao waweze kuondoka bila ya kuwa na madai mengine yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo nilikuw anataka kuchangia bado ni kuhusiana na madeni ya Madiwani; wenzangu wamezungumzia sana na mimi ni kwamna jamani Madiwani wetu waweze kulipwa yale madeni yao ya posho na stahiki zao nyingine pamoja na Watumishi hii inawapa motisha ya kufanyakazi vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna madeni pia ya wazabuni; wazabuni wameweza kzilisha Halmashauri zetu, wamefanya zabuni mbalimbali lakini wanakuwa wanadai muda mrefu na tunajua kwamba hawa wazabuni ndiyo wafanya biashara ndiyo tunawategemea tupate kodi zao sasa kama tukiwa-paralysis wakapoteza biashara zao bado tutakuwa hatujawasaidia. Mheshimiwa Rais amekuwa akisema hawa watu ndiyo wa kuwasaidia maana yake ni watu ambao tunatakiwa na wenyewe tunategemea tuwakamue yaani tuwape maziwa na tukamua, tupate kodi nyingi za kutosha. Kwa hiyo, ningeomba hili pia Serikali ingeliweka vizuri ili kusiwepo na madeni makubwa sana ya Wazabuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ni uhaba wa Watumishi katika halmashauri zetu; wahasibu, walkaguzi, wakuu wa idara lakini ni muhimu sasa Halmashauri au Serikali kuna mamlaka mpya kwa mfano; RUWASA, TARURA wanatoa wale watalam kwenye halmashauri zetu wanapelekwa kwenye hizo Taasisi, kwenye mamlaka lakini kwenye halmashauri sasa tunakuwa hatuna wale wataalam. Kwa hiyo, utakuta halmashauri nyingi hazifanyi vizuri hata kwenye miradi, hakuna wale wataalam. Kwa hiyo, ningeomba pengine hili lingewekwa voizuri kwamba wanapotolewa tu wataalam wowote basi mara moja Halmashauri wanaziba yale mapengo ili ziendelee kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine nizungumzie kuhusu Serikali kupeleka pesa katika miradi ya kimkakati katika Halmashauri zetu; kumekuwa na tatizo kubwa la kuchelewesha hizi pesa za miradi ya kimkakati pamoja na kuwa na nia nzuri sana ya halmashauri kwamba miradi ya kimkakati isaidiwe ili iweze kusaidia mapato katika halmashauri lakini utakuta miradi imekuwa ya muda mrefu sana kwa hiyo sasa inatia tu hasara lakini tulikuwa tunategemea kwamba kama huu mradi ungepewa pesa kwa wakati ule pengine ungefanyika upembuzi yakinifu, kuna miradi mingine inahitajika pesa kidogo sana ingekuwa imeshakamilika. Kwa mfano; tuna mradi wa machinjio pale kwetu ni wamuda mrefu, mashine zimefungwa muda mrefu mpaka zinaweza zikapata kutu laklini kwa mfano mkitoa pesa tu kidogo ule mradi utaleta mapato makubwa kwenye halmashauri kwa hiyo utasaidia mapato na mambo mengi yatakwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumza hayo niendelee kuwapongeza Mawaziri wote waliopo TAMISEMI na wafanyakazi wote na Kamati zote ambazo zimewasilisha report zao hapa lakini na ambayo tumeyatolea ushauri basi yafanyiwekazi ili tuendelee na maboresho lakini nampongeza pia Mheshimiwa Rais kwa akzi kubwa amabyo amekuwa akiifanya katika nchi yetu na Chama cha Mapinduzi kwa utekelezaji wake wa ilani. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya kilimo. Kwanza kabisa naomba nichukue nafasi kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Manaibu wote Mawaziri wa Wizara hii kwa kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya kwa kipindi kifupi ambacho wamekuwa katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na muda kuwa mchache, naomba niende moja kwa moja kwenye hoja. Kwanza kabisa nichangie kuhusiana na changamoto katika vituo vya utafiti. Kwa kweli mimi ni mjumbe, tumetembelea katika hivi vituo, hali ya vituo ni mbaya mno. Ningeomba Serikali sasa itambue umuhimu wa vituo vya utafiti, ili sasa tuweze kufanya utafiti wa uhakika katika mbegu, magonjwa, dawa za tiba, viuatilifu, udongo, ili tuweze kutenda haki kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, nizungumzie kuhusiana na NDC, inafanya kazi nzuri sana za kuwakopesha wakulima zana za kilimo za kisasa. Je, wakulima wanatambua kuhusiana na haya matrekta kwa sababu, ni bei rahisi na tunategemea kwamba, kama wakulima watapata matrekta yatasaidia kulima kilimo cha kisasa ambacho kitaleta tija katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini moja kwa moja niende katika Mkoa wangu wa Iringa kuhusiana na zao la pareto. Hili ni zao la biashara katika Mkoa wetu wa Iringa, linatuingizia pato katika mkoa wetu na katika nchi hii, lakini kuna kiwanda ambacho kiko katika Wilaya ya Mufindi. Vilevile tushukuru kwamba, katika hiki kiwanda kinahitaji kama tani 5,000 za maua ya pareto, lakini kuna walanguzi ambao wamekuwa wakija kuwarubuni wakulima katika hili zao la pareto kwa sababu, sasa hivi kiwanda kinapata maua kama tani 2,500 tu na kiwanda tushukuru kwamba, wamekuwa wakiwa- support wakulima kwa kuwapa pembejeo na utaalam, tuwapongeze sana, lakini sasa je, Serikali inalindaje viwanda kama hivi na inalindaje wakulima?

Mheshimiwa Spika, inalindaje kuhakikisha kwamba, walanguzi hawaji kulangua malighafi katika maeneo ambayo wakulima wanafanya maana tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda. Sasa kama Serikali itakuwa haina mpango mzuri, mkakati wa kuhakikisha kwamba, inalinda hivi viwanda bado tutakuwa tunapiga mark time. Sasa niombe je, hakuna sheria inayolinda viwanda ambavyo vinawekeza katika nchi yetu?

Mheshimiwa Spika, vilevile nizungumzie kuhusiana na masoko. Tatizo kubwa la mkulima ni masoko. Nyanda za Juu Kusini tunalima mahindi, pareto, parachichi, viazi, lakini mkulima leo hii anapolima hajui soko atalipata wapi, lakini kuna Bodi ya Mazao Mchanganyiko ambayo tulikuwa tunategemea kwamba, sasa itatusaidia kututafutia masoko, lakini bado unaona kwamba ina changamoto kubwa sana, haipatiwi fedha za kutosha kuhakikisha kwamba, inafanya kazi inayotakiwa; sasa je, Serikali mmejipangaje? Maana bila soko bado wakulima wetu wamekuwa maskini.

Mheshimiwa Spika, mkulima wa leo hawezi hata kumsomesha mtoto. Mkulima wa leo yani analima, lakini wanaofaidika ni wale walanguzi. Sasa ifike sehemu Serikali hii imwezeshe mkulima, ili ajisikie kama wakulima walivyo katika nchi nyingine wanapata heshima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie Benki ya Kilimo; Benki ya Kilimo tulikuwa tunategemea itusaidie katika kuhakikisha kwamba, mkulima anakopesheka, kwa sababu, mkulima wa sasa hivi hakopesheki kutokana na risk kubwa ambazo anazo. Tuombe kwamba, bima ya mazao iwekewe udhibiti, ili aweze kukopesheka, lakini tuombe benki hii iongezewe mtaji wa kutosha...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Dkt. Kigwangala, Naibu Waziri Mheshimiwa Kanyasu, Makatibu Wakuu na viongozi wote wa Wizara kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Naomba mchango wangu ujikite katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Regrow; naipongeza Serikali kwa kutoa kipaumbele na kuona umuhimu wa kuendeleza utalii Kanda ya Kusini (Regrow). Mradi huo unalenga kuongeza ubora wa vivutio vya utalii Kusini mwa Tanzania ikiwa ni pamoja na kuimarisha fursa za kiuchumi kwa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ukiwemo Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali kwa kuanza kutua ndege kubwa aina ya Bombadier katika Kiwanja cha Ndege cha Iringa. Pamoja na hilo ni vyema sasa Serikali ikaboresha kiwango cha lami barabara inayokwenda katika Mbuga ya Wanyama ya Ruaha, mbuga ya pili kwa ukubwa katika Afrika na ina wanyama wengi. Wizara hii ya Utalii inatoa msukumo gani kwa Wizara ya Ujenzi na kuona hiyo barabara inaharakishwa kujengwa kwa sababu imechukua muda mrefu sana kutangazwa ujenzi, lakini haufanyiki. Naomba kujua ni elimu kiasi gani inatolewa ili kuwaandaa wananchi wanaozunguka Mradi huu wa Regrow wanaandaliwa ili kujiajiri kupitia utalii?

Mheshimiwa Naibu Spika, Ongezeko la Watalii nchini; niipongeze Serikali kwa kufanya jitihada na kusababisha watalii kuongezeka kutoka 1,327,143 mwaka 2017 na kufikia 1,505,702 mwaka 2018 na kuongeza pato la Taifa, lakini ningependa kujua mkakati wa kuhakikisha watalii wengi wanafika katika mikoa yetu ambako kuna vivutio vingi ambavyo bado hatujaona kutembelewa na watalii wa kutosha katika Mkoa wetu wa Iringa. Je, Serikali imejipangaje kuajiri Maafisa Utalii kila Halmashauri, Wilaya na Mikoa kwa sababu, kuna Halmashauri nyingine zina vivutio vingi, lakini hakuna Maafisa Utalii kuna Maafisa Misitu tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Waziri Mheshimiwa Japhet Hasunga, Naibu Mawaziri Mheshimiwa Bashungwa na Mheshimiwa Mgumba pamoja na Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kuwasilisha hotuba ya bajeti hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kupongeza Serikali kwa usajili wa wakulima; jambo hili ni jema sana. Ni imani yangu sasa zoezi hili la usajili wa wakulima nchini Serikali itaweza kutambua:-

(i) Ardhi itakayotumika katika kilimo

(ii) Mahitaji halisi ya wakulima kama mbolea, mbegu, madawa na viuatilifu, upangaji wa bajeti utarahisishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini naitaka kujua, je, hili la usajili litachukua muda gani kukamilika na linafanyikaje? Je, uelewa wa wakulima katika kujisajili ukoje?

Mheshimiwa Spika, miradi ya umwagiliaji; hadi kufikia mwaka 2017, jumla ya skimu 2,942; skimu zilizoendelezwa zipo 960 tu na skimu ambazo bado hazijaendelezwa zipo 1,987 na katika Mkoa wetu wa Iringa una jumla ya skimu 58 za umwagiliaji. Hapo ni lazima tukiri Tume ya umwagiliaji haikufanya vizuri katika kipindi kilichopita. Hivyo, niipongeze Serikali kwa kuona umuhimu wa kuondoa baadhi ya watendaji katika Tume hiyo na kuunda Tume mpya. Ni vyema sasa Serikali ingefanya upembuzi yakinifu wa miradi ile iliyokaribia kumalizika au miradi yenye tija ili ipatiwe kipaumbele kupatiwa pesa kuliko kutoa pesa kidogo kidogo katika miradi mingi matokeo yake huwa inakuwa miradi haikamiliki mingi na pesa inapotea bila tija yoyote. Pia Benki ya Kilimo na Mfuko wa Pembejeo watoe asilimia 20 kusaidia miradi ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, Maafisa Ugani; asilimia 25 ya wakulima wadogo nchini ndiyo wanapata mbegu bora na asilimia 10 ya ardhi inayolimwa ndiyo inatumia mbolea, lakini uajiri wa Maafisa Ugani na mazingira ya kazi vimekuwa ni changamoto kubwa sana nchini. Mfano, kati ya mwaka 2014 - 2016, Maafisa Ugani waliopata mafunzo na kuhitimu walikuwa 3,189 lakini kati ya hawa, asilimia 20 tu ndiyo walipata ajira. Upungufu wa vituo vya kuwapatia maarifa wazalishaji wadogo na uwezo mdogo wa rasilimali (wataalam wa teknolojia). Je, nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha Maafisa Ugani wanaajiriwa?

Mheshimiwa Spika, Benki ya Kilimo; tunapongeza kwa kuzindua Benki ya Kilimo. Benki hii itakuwa ndiyo mkombozi kwa wakulima nchini na vizuri Serikali itoe ruzuku ya kutosha kwa Benki hii kwa sababu kushuka kwa mikopo sekta ya kilimo kulinganisha na sekta nyingine, hii inatokana na taasisi za fedha kuchukua kilimo kama sekta hatarishi (risk) na uanzishwaji wa Bima ya mazao utasaidia wakulima wetu kukopesheka kama kutakuwa na ukame, mafuriko, uvamizi wa viwavi jeshi na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, changamoto katika vituo vya utafiti; tulifanya ziara katika vituo vya utafiti hali ni mbaya sana. Bila Serikali kuona umuhimu wa kutenga pesa ya kutosha ili tafiti ziweze kufanyika hata sera yetu ya uchumi wa viwanda itakuwa kazi bure sababu viwanda vyetu vitakosa malighafi ya uzalishaji. Mfano, mbegu tu ya mahindi ni asilimia 65 kutoka nje, mboga mboga asilimia 99 kutoka nje. Serikali ingewekeza katika Taasisi ya ASA wakawekewa miundombinu ya umwagiliaji, matrekta na zana za kilimo, hiki kituo kingeweza kuzalisha mbegu za kutosha.

Mheshimiwa Spika, zao la pareto; hili ni zao la biashara katika Mkoa wetu wa Iringa. Pia kipo kiwanda katika Wilaya ya Mufindi. Kiwanda kina uhitaji wa maua ya pareto kiasi cha tani 5,000, lakini wakulima wana uwezo wa kuzalisha tani 2,500 tu. Tunawapongeza sana wamiliki wa Kiwanda cha Pareto kwa kuwapatia wakulima pembejeo na utaalam, lakini mbaya zaidi kuna walanguzi wanaokuja kuwarubuni wakulima maua yao. Je, Serikali inalinda vipi viwanda vyetu nchini dhidi ya hawa walanguzi? Hata tulipofanya ziara katika mashamba ya parachichi Mkoa wa Njombe kulikuwa na changamoto ya walanguzi toka nchi jirani kuwarubuni wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. DKT. RITHA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kuhusu Azimio la Bunge Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Kuhusu Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri wa Kilimo na watendaji wote kwa kuwasilisha Azimio hili ili tuweze kulijadili. Nimpongeze pia Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Kilimo na Wajumbe wa Kamati ya Kilimo kwa maoni na ushirikiano wao walioutoa kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa mmojawapo wa wajumbe wa Kamati, kama Kamati tuliweza kukutana na wataalamu mbalimbali ili kuhoji na kujiridhisha. Pia, tuliweza kupitia na kuchambua na kuona faida na hasara za kupitisha Itifaki hii. Zipo baadhi ya faida tuliona kama kukuza na kuimarisha biashara ya chakula na mazao ya kilimo na mifugo; kupunguza vikwazo visivyo vya kiforodha mipakani; kuongeza hamasa miongoni mwa wakulima katika kuongeza viwango vya ubora wa bidhaa na mengine mengi ambayo Mheshimiwa Mwenyekiti wetu amewasilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uridhiwaji wa Itifaki hii, Kamati ilibaini upungufu katika mifumo ya usimamizi wa taasisi mbalimbali zinazohusika na afya ya mimea. Ni vyema Serikali ikazingatia ushauri uliotolewa na Kamati ili kuondoa upungufu huo. Pia, kuandaa sera mahsusi inayosimamia usalama wa chakula na kuhuisha sheria mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kuhuisha sheria mara kwa mara kwa sababu kuna wakati tulifanya ziara Kanda ya Ziwa na yapo mapungufu ya kisheria ambayo tuliyaona mfano katika Ziwa Viktoria, kulikuwa kuna sheria ambazo zimewekwa kwa ajili ya nchi wanachama lakini tuliona zile sheria kwa upande wetu zilikuwa hazihuishwi mara kwa mara na kusababisha kwamba nchi yetu pamoja na kuwa nchi yetu ndiyo inamiliki eneo kubwa katika Ziwa Viktoria lakini wenzetu walikuwa wanapata faida kutokana na zile sheria ambazo zilikuwa zinawabana wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hasara iliyokuwa inapatikana ni kwamba wafanyabiashara wengi walifunga viwanda na kwenda kufungua viwanda Uganda na Kenya. Kwa hiyo, ilikuwa inasababisha nchi yetu kukosa viwanda na ajira kwa sababu kufungwa kwa viwanda vijana wetu wengi walikuwa wanakosa ajira. Kwa hiyo, naomba tunaporidhia Itifaki hii Serikali ijipange kuhuisha sheria mara kwa mara na iwe flexible ili wenzetu wanapohuisha sheria zao na sisi tuhuishe za kwetu kwa ajili ya manufaa ya nchi yetu na wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Itifaki hii imezingatia maslahi mapana ya Taifa na nchi yetu ikiwa ni mnufaika mkubwa wa Itifaki hii kutokana na kuwa ndiye mzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na mifugo miongoni mwa nchi wanachama. Pamoja na kuwa tulikaa miaka nane bila kuidhinisha Itifaki hii, sasa imefika wakati muafaka nchi yetu iweze kuidhinisha itifaki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na nimpongeze Waziri wa Fedha, Dkt. Mpango, Naibu Waziri Dkt Kijaji, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na kuwasilisha bajeti na taarifa ya hali ya uchumi wa Taifa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijatenda haki kama nitakuwa sijampongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana. Kwa kipindi kifupi ameweza kusimamia ukamilishwaji wa miradi mikubwa sana ya maendeleo. Pia kwa kikao kizuri sana alichokifanya tarehe 7/6/2019 Ikulu na wawekezaji na wafanyakazi nchini. Mheshimiwa Rais ameonyesha jinsi anavyoweka kipaumbele katika kuchochea uwekezaji nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze Serikali pia kwa kuona umuhimu wa kusikiliza kero na kuondoa tozo 54 za kodi mbalimbali, lakini pia Serikali iangalie mwingiliano wa majukumu ya taasisi au mamlaka za udhibiti kama TBS, TFDA na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie kuhusu madai ya watoa huduma kwa Serikali yanachukua muda mrefu kulipwa wakati wazabuni hao pia wanatakiwa kulipa kodi zao Serikalini kwa wakati.

(i) Kwa nini kusiwepo na utaratibu wa kubadilishana madeni, yaani Serikali ichukue kodi yake inayodai wazabuni kutoka kwenye deni inayodaiwa na mzabuni, hivyo kupunguza mzigo wa kulipa pesa ambayo mzabuni bado hajalipwa.

(ii) Mtoa huduma anapotoa huduma kwa taasisi zikiwemo zile za Serikali anatakiwa aambatanishe invoice yake ya madai na receipt ya EFD hii ikiwa na kuwa analipa kodi ya VAT hata kabla ya kupata malipo husika. Kwa nini EFD isitolewe pale tu malipo ya huduma yanapofanyika na si wakati wa madai yanapowasilishwa ikiwa na maana ni kwa malipo ya huduma kwa yanayochelewa kulipwa? Hivyo huathiri mitaji ya mfanyabiashara na kuanguka kwa biashara hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo miradi ambayo ni ya kimkakati lakini Serikali inachelewesha kupeleka pesa na kusababisha gharama za miradi kuongezeka kwa kiasi kikubwa sana mfano, katika Mkoa wa Iringa upo mradi wa machinjio ya kisasa, mradi huo una zaidi ya miaka 10 toka uanzishwe na mradi huu kama ungekamilika kwa wakati ungeweza kuwa ni chanzo kizuri sana cha mapato katika Halmashauri yetu na ni mradi ambao ungetengeneza ajira zaidi ya 200 kwa wananchi wa Iringa. Ni kwa nini Serikali isifanye upembuzi yakinifu wa miradi kama hii nchi nzima na kuipatia fedha ili halmashauri zetu ziweze kujiendesha?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaelekea katika uchumi wa viwanda nchini lakini barabara nyingi bado wakati wa kipindi cha masika hazipitiki kabisa. Ni kwa nini Serikali isifanye upembuzi yakinifu wa barabara zote za kiuchumi ili itoe kipaumbele kutokana na bajeti finyu ya TARURA zihudumiwe na TANROAD. Kwa mfano, Mkoa wetu wa Iringa karibu barabara zote wakati wa masika hazipitiki kabisa na kusababisha magari makubwa yanayobeba mazao ya misitu kukwama karibu siku tano mpaka saba au zaidi na kuleta athari kubwa sana za kiuchumi. Pia mkoa wetu unategemewa hata kuwa na malighafi za viwanda na wakulima wanashindwa kufikisha sokoni mazao kama njegere, mahindi, vitunguu, nyanya, viazi na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. RITTA R. KABATI: Mheshimiwa Spika, Ahsante naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi lakini moja kwa moja niende kwenye point nimshukuru Mwenyezi Mungu, nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi lakini pia niwashukuru wajumbe walionichaguwa nikiwemo humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake aliyotoa hapa Bungeni kwa sababu kwanza alitoa dira na maelekezo nini tufanye na na Serikali nini ifanye kwa hiyo kwetu sisi kazi yetu kufanya.

Mheshimiwa Spika, hotuba ambayo imekuwa elekezi kwa viongozi wote vilevile naomba nichukue nafasi kupongeza ya uchaguzi kwa kusimamia zoezi lile vizuri kwa kuwa uchaguzi ulikuwa uhuru na haki na viongozi wote walioingia humu ndani wameingia kwa uhuru na haki, niwapongeze Wabunge wote wa Chama cha Mapinduzi lakini pia wa vyama vya upinzani kwa sababu wote tunajenga nyumba moja.

Mheshimiwa Spika, naomba moja kwa moja nielekeze katika miradi ya maji kwa sababu sisi ni Wabunge Wanawake ambao tunawakilisha wanawake tumeona hotuba hii imelenga moja kwa moja kuhusiana na miradi ya maji. Ujenzi wa miradi ya maji imefanya wanawake wengi sana sasa hivi hawahangaiki kutafuta maji, tunaona kwamba katika Mkoa wetu wa Iringa kulikuwa na tatizo kubwa hasa miradi ya vijijini kwamba miradi ya Kilolo, kule Mufindi, Isimani, wanawake walikuwa wanapata shida sana hata katika Mkoa wetu wa Iringa unaona maji yalikuwa yanatuletea adha kubwa, kuna ndoa nyingi sana ziliweza kupata matatizo kwa sababu maji ni uhai, lakini mwanamke anaamka asubuhi time ambayo anatakiwa ailinde ndoa yake anaenda kuiangaikia maji. Kwa hiyo, kwa kweli Mheshimiwa Rais amelinda hata ndoa zetu katika Mkoa wetu wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tu hata mimi nitowe ushauri kwamba Serikali sasa hivi ianze kuangali uvunaji wa maji kwa sababu maji kumekuwa na upotevu wa maji mkubwa, tukitengeneza miundombinu ya kuvuna maji hasa katika mabwawa tutasaidia hata mifugo yetu wakati ule hakuna mvua itapata maji, lakini vilevile tunaona kwamba hizi mvua zimekuwa zikija na mafuriko makubwa, kwa hiyo, tukivuna haya maji yatasaidia pia kuzuia uharibifu katika mito yetu, lakini pia hata mabarabara na madaraja wakati wa mvua za masika.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusu suala la afya niipongeze sana Serikali yetu imeweza kujenga zahanati 1,998, vituo vya afya 487, Hospitali za Wilaya 96, Hospitali za Kanda tatu lakini maboresho ya afya yamesababisha hata kupunguza vifo vya akinamama na watoto. Tunaona mwaka 2015 vifo vilikuwa 11,000 lakini sasa hivi mwaka 2020 unaona vifo vingi vimepungua vimefikia mpaka vifo 3,000 kwa mwaka, hii yote ni kwa sababu ya maboresho mazuri ya vituo vya afya, lakini vilevile Serikali ihakikishe kwamba inaweka watumishi kwenye vituo vya afya, inaleta madawa ya kutosha, lakini naomba ili kupunguza vifo vya watoto njiti iwekeze kwenye vituo vya afya kwa sababu tunaona katika vituo vya afya hakuna zile incubator kwa ajili ya watoto, watoto wengi sana wamekuwa wakipoteza maisha katika vituo vya afya, kwa hiyo naomba sasa Serikali iwekeze sana kwenye vituo vya afya mambo incubator.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye ukurasa wa 27, imezungumzia kuhusu kilimo, Serikali inakusudia kuongeza tija na kufanya kilimo kuwa cha biashara. Karibu asilimia 75 ya Watanzania ni wakulima, kwa hiyo, tukiwekeza kwenye kilimo ina maana kwamba sasa hivi tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda na kwenye kilimo ndipo ambapo tutapata malighafi. Kwa hiyo, kwa kweli tukiondoa changamoto nyingi ambazo zipo kwenye kilimo, ndipo ambapo tunaona hata Mheshimiwa Rais amesema kwamba ni aibu kubwa kuwa na njaa kwenye nchi yetu. (Makofi)

Lakini sasa hivi nchi yetu ya Tanzania ina uwezo hata wa kupeleka vyakula katika nchi nyingine. Lakini kuna mkakati mahususi kuhakikisha kwamba sasa hivi…

(Hapa kengele ililia kaushia kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mpango wa Tano wa Maendeleo. Naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia, kwanza kabisa nianze na kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kupata tuzo na kushika nafasi ya pili kwa kiongozi bora wa Marais katika Afrika, akiongozwa na Rais wa Ghana. Tuzo hiyo imetolewa na African Leadership ambayo Makao Makuu yake yako London, kwa kweli, nani kama Magufuli? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo niendelee kumpongeza pia Mheshimiwa Mpango kwa kutuletea Mpango wake ili tuweze kuuchangia hapa Bungeni. Pia, nimpongeze hata Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kwa kuweza kuwasilisha mpango vizuri katika Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda. Katika kuelekea kwenye uchumi wa viwanda ni muhimu sana Mpango wetu ujikite kuhakikisha kwamba, barabara za kiuchumi zinapitika wakati wote, kwa sababu barabara zetu nyingi hazipitiki wakati wa mvua. Kwa hiyo, niiombe Serikali yetu ifanye upembuzi yakinifu kuhakikisha barabara zile za kiuchumi zinapitika na ikiwezekana zijengwe kwa kiwango cha lami, ili tuweze kupeleka malighafi katika viwanda vyetu. Vilevile kupunguza vifo vya akinamama na watoto katika maeneo yetu hasa ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano katika Mkoa wetu wa Iringa, zipo barabara za kiuchumi ambazo kwa kweli wakati wa masika hazipitiki. Mheshimiwa Kihenzile jana alikuwa anachangia na akataja baadhi pia ya maeneo ambayo hayapitiki kabisa na sasa hivi kuna malori yamekwama karibu wiki nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye baadhi ya barabara zetu za kiuchumi; kuna barabara ya Nyololo - Mtwango kama kilomita 40; ya Mafinga - Mgololo, Mafinga – Mapanda; Ipogolo – Kilolo; na Kilolo – Idete. Hizi ni baadhi tu ya barabara za kiuchumi ambazo tuna imani kabisa kama zitafanyiwa kazi vizuri pato la Taifa litaongezeka kwa sababu magari yatapita muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuchangia kuhusiana na mradi wa REGROW ambao ni mradi wa kuendeleza maliasili na kukuza utalii Kusini mwa Tanzania. Mradi huu ulikuwa unatekelezwa na fedha za World Bank na utafaidisha Mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya, Songwe, Katavi, Rukwa pamoja na Ruvuma na Makao Makuu yake ni Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kuutambulisha mradi huu ulikuwepo na ulikuwa mgeni rasmi lakini hatujaona maliasili na utalii katika Mikoa yetu hii ya Kusini tunafanyaje huu utalii? Tulikuwa tuna imani kabisa huu mradi ungesaidia kuleta ajira nyingi sana kupitia utalii na pato la Mikoa yetu ya Kusini na tulitegemea tuanze mashindano kati ya Mikoa ya Kaskazini na Kusini ili tuweze kupata kipato kikubwa cha taifa kupitia miradi ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka kujua, je, Maliasili sasa wamejipangaje? Huu mradi unaanza lini? Kabla hatujapata hizi fedha, je, wanatangaza, maana yake biashara ni matangazo, wanatangaza vivutio vilivyopo katika maeneo yetu ya Kusini? Vivutio Kusini viko vingi sana na siku ile ulishuhudia Wakuu wa Mikoa wote walieleza vivutio vizuri sana katika kila mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sasa Serikali ianze kutumia hata pato la ndani kabla ya kupata hizi fedha tuhakikishe tunatengeneza vivutio vyetu ili viweze kupitika tupate watalii wa ndani na wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono 100% Mpango huu wa Taifa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili nichangie hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza, naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu lakini niseme Ramadhan Kareem kwa Waislam wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Waziri Mkuu na Mawaziri wote walioko katika Wizara yake bila kumsahau Mheshimiwa Jenista Mhagama. Kwa kweli wananchi wa Iringa wanasema kwamba mambo makubwa yaliyofanyika katika Mkoa wetu wa Iringa hatuwezi kumsahau Dkt. John Pombe Magufuli. Amefanya mambo makubwa ambayo hata kuyasimulia tunashindwa. Wameniambia niseme tu neno moja, gendelage ludodi baba, gendelage ludodi, Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na wote waliochangia kuhusu TARURA kupatiwa fedha za kutosha. TARURA ndiyo ambayo inahudumia barabara nyingi sana za vijijini ambazo ndizo zina matatizo mengi. Kwa mfano, Mkoa wetu wa Iringa mtandao wa barabara za TARURA ni karibu kilometa 4,597.9 na una mvua nyingi sana, milima, maporomoko, hivyo, TARURA inatakiwa iwe na pesa nyingi kwa ajili ya kujenga madaraja, makalvati kwa sababu barabara nyingi zimeharibika. Hizi barabara ni za kiuchumi zinapitisha mazao ya misitu ambapo magari ni mazito yanafanya barabara hizi zinakuwa hazipitiki wakati wa mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitende haki, nitaje baadhi ya barabara ambazo sasa hivi hazipitiki. Katika Wilaya ya Mfindi kuna hii barabara Mtiri – Ifwagi - Mdabulo - Kilosa haipitiki kabisa. Kuna barabara ya Ibwanzi – Lulanda; Nyololo – Mtwango; Mafinga - Mgololo, hizi barabara Mufindi wanapata mateso makubwa mno. Ukienda kwenye Wilaya ya Kilolo kuna barabara ya Boma la Ng’ombe – Jingula. Kata ya Masisiwe, kuna Kata ya Nyanzwa, Kijiji cha Mahenge na Magana kuna madaraja mawili yamekatika kiasi mtandao wa barabara hakuna kabisa. Ukienda katika Jimbo la Kalenga kuna barabara ya Lumuli – Magungu – Magulilwa - Nyenza, hizi barabara ni mateso makubwa sana kwa wananchi wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipokwenda kuwatembelea wakwe zangu kule Mwanza nilikuta kuna barabara pale Ilemela za VETA – Igombe TX; Airport - Nyagugi kama kilometa 18, toka nimeolewa bado hazijafanyiwa kazi yoyote. Naomba Waziri atusaidie kuziangalia barabara hizi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusu walimu wanaohitimu katika vyuo vyetu vya elimu. Tunao walimu ambao kwa kweli wamekuwa wakijitolea mara nyingi hasa katika Mkoa wa Iringa hata katika maeneo mengine lakini zinapokuja ajira hawaajiriwi. Pamoja na kuwa Mkoa wetu wa Iringa umefanya vizuri sana katika elimu, tumekuwa tatu bora na hawa walimu wanachangia kwa sababu wamekuwa wanajitolea kwenye masomo ya sayansi na hisabati. Niombe Serikali iwape kipaumbele, hii itasaidia hata wengine kuwa na moyo wa kujitolea hata kama wamemaliza masomo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze pia kuhusu watu wenye ulemavu. Nishukuru Serikali kwamba imetoa ile sheria kwamba watu wenye ulemavu angalau kila mtu aweze kupata ile asilimia mbili. Hata hivyo, kuna wamama wengi ambao wamezaa watoto wenye ulemavu ambao kwa kweli wanapata matatizo makubwa sana kuwalea wale watoto kwa sababu wengi wamekimbiwa na waume zao unakuta wao ndiyo wanahudumia wale watoto kuanzia masomo na malezi. Niombe labda ile asilimia mbili na wenyewe wangepatiwa ili hawa watoto waweze kusomeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni uhaba wa watumishi katika sekta ya afya. Vimejengwa vituo vya afya na hospitali nzuri sana ila kuna uhaba mkubwa sana wa watumishi katika sekta ya afya. Nikichukulia tu mfano Kilolo tuna hospitali ya mfano, ni nzuri sana na imeshakamilika lakini kuna upungufu wa watumishi 93. Wilaya hii kwa ujumla ina upungufu wa watumishi katika sekta ya afya kwa asilimia 40. Niombe kwamba tunapokamilisha hivi vituo vya afya basi iendane na kukamilisha kabisa watumishi kwa sababu bado unaona wananchi wanapata shida sana kwenda kutafuta huduma wakati tayari tumeshajengewa vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu wazee. Wazee ni dawa na baraka lakini wamekuwa na changamoto nyingi sana. Niombe Serikali iangalie changamoto za wazee. Hata leo imezungumziwa kuhusu matibabu ya wazee na nishukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja kwenye kongamano la afya za wazee katika Mkoa wetu wa Iringa na wanakushukuru sana. Lile kongamano lilifanya tukajua changamoto nyingi za wazee, wazee hawahitaji dawa wakati mwingine wanahitaji kuangaliwa wajijue kwamba wanahitaji kula lishe, kufanya mazoezi au faraja. Wazee wengi sasa hivi wameondolewa kulipia kwenye nyumba zao lakini bado wanalipa kodi ya ardhi. Naomba pia ile kodi ya ardhi itolewe kwa sababu tumeshawaondolea kulipia kodi ya nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Bima ya Afya labda sasa izingatie ili wazee wetu waweze kutibiwa, kuchekiwa afya ya macho na vipimo vyote. Pia wanahitaji kupewa dawa lakini hazitoshi na leo lile swali limeeleza mambo makubwa sana kuhusu wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nizungumzie kuhusu matatizo ya maji kwenye Mkoa wa Iringa. Nishukuru sana kwamba Wizara ya Maji inafanya vizuri sana mijini lakini bado vijijini wamama wengi wanapata shida. Mkoa wetu wa Iringa una mito mingi; Mto Lukosi, Mto Ruaha ila kule vijijini maji hakuna. Ni kwa nini wasivute maji ili wananchi wa Iringa wapate maji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda umekwisha.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Mheshimiwa Mama Samia, kwa kweli akina mama tunaweza na tunashukuru baba yetu alimteuwa akawa Makamu wake.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati muda wako umeisha.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nakupa big up, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami nichangie kuhusiana na hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwanza kwa kumpongeza Waziri wa Sheria na Katiba pamoja na Naibu Waziri na Watendaji wote wa Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kupongeza Bunge lako, kukupongeza wewe na Mheshimiwa Spika kwa ajili ya kutunga Sheria ya Matumizi ya Kiswahili katika Mahakama zetu na vyombo vingine vya utoaji haki. Kwa kweli kutunga sheria huku kumesaidia sana wananchi wengi kupata haki kwa sababu wengi walikuwa wanahukumiwa kwa kutojua tu lugha inayozungumziwa katika Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie kuhusiana na kesi za ubakaji hasa katika Mkoa wetu wa Iringa. Tuna kesi zaidi ya 400 katika mkoa wetu, lakini naona zinachukua muda mrefu sana. Nilikuwa najiuliza ni kwa nini kesi hizi zisiwe na limit? Kwa sababu kuna nyingine ambazo zinakuwa tayari zimeshakuwa na vidhibiti, lakini tunaona kwamba zinachukua muda mrefu. Kesi hizi zimekuwa zikiwadhalilisha sana watoto na hata akina mama wanaobakwa, kwa sababu zimekuwa zinanyima hata haki zao za binadamu kwa kuchukua muda mrefu. Sasa naona ifike sehemu ziwe na time limit. Ziwekewe limit za kuhukumiwa hizi kesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie kuhusiana na msaada wa kisheria. Pamoja na kuwa nimeona kwamba limezungumziwa katika hotuba ya Waziri, lakini bado msaada wa kisheria umekuwa ukiwanyima wananchi wanaoshindwa kuweka Wakili kwa ajili ya kupatiwa haki. Sasa tulipitisha hapa Bungeni kwa nia nzuri kabisa na tulikuwa tunajua kwamba baada ya kupitisha, zile changamoto pengine zingeweza kukamilika kwa wakati, lakini unaona bado kabisa wananchi wanakosa msaada wa kisheria na wanakosa haki zao na kwa sababu wanashindwa kuweka Wakili kwa ajili ya kuwatetea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tathmini ifanyike katika mikoa na hasa sehemu ambazo zina kesi nyingi, kwa mfano mkoa wetu wa Iringa ambao una kesi nyingi sana na tunaona kuna mashirika ambayo yanasaidia msaada wa kisheria, lakini bado wananchi wanalalamika kwa kukosa haki kwa kutokuwa na Wakili wa kuwatetea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia pale Mkoani kwetu Iringa kuna changamoto. Tuna kesi nyingi sana za mauaji ambazo kutokana na kutokuwa na fungu la kutosha kuendesha hizi kesi, basi unaona wale wafungwa kule mahabusu wanakaa muda mrefu, kesi hazikamiliki. Naomba kesi za mauaji pia zipewe kipaumbele, fungu lipelekwe ili zihukumiwe haraka. Kama mtu amefanya kosa, basi aweze kuhukumiwa na kama hana hatia aweze kuondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusiana na sheria kandamizi kwa wanawake. Wanawake wengi wanakandamizwa sana kwenye mambo ya mirathi, ndoa, talaka; maeneo haya matatu tunaona yanaongoza, hasa kuna sheria tatu. Kwanza, kuna sheria ambayo tumekuwa tukiitunga hapa Bungeni kuna sheria nyingine ni za kidini na sheria za kimila.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria za Bunge siyo mbaya sana, lakini sheria za kidini sitaki kuzisema kwa sababu zenyewe zinaenda kiimani zaidi. Sheria ambazo ni kandamizi ni hizi za kimila kwa sababu zinafuata mfumo dume kwa kuwa zimejikita sana katika mila na desturi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali ni je, Sheria za Kimila haziwezi kurekebishwa ziendane na wakati? Ni dhahiri kuwa Sheria hizi za Kimila utaona nyingi sana zinafafana, yaani hazipo uniform katika kila maeneo. Kwa kutambua hilo, nafikiri sheria zilizoingizwa kwenye sheria ya kimila ndani ya mfumo wa Sheria za Tanzania (Judicature and Application of Laws Act) ya 11 na 12 zimeeleza kwamba Halmashauri za Wilaya ziwe na utaratibu wa kupitia hizi sheria na maeneo ya halmashauri zao, lakini tunaona bado halmashauri nyingi hazijaweza kuzipitisha hizi sheria za kimila. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaona sasa wanawake wengi sana na hata watoto wanapata shida kwa sababu sheria hii bado haijaweza kupitiwa ili iendane na mila na desturi ambazo wananchi tumo. Je, sasa ni lini Waziri wa Sheria ataweka huu mfumo kwamba ziweze kupita katika halmashauri zetu ili zitendr haki kwa wananchi ambao tunaoishi nao?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja kuhitimisha hoja yake hapa, atueleze kwa sababu hizi Sheria za Kimila zimekuwa zikimkandamiza sana mwanamke kwenye mambo mengi, kwenye mirathi na mambo mengi sana. Kwa hiyo, naomba atakapokuja hapa kutuelezea, aelezee kuhusiana na hii Sheria ya Kimila kuingizwa katika sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nielezee kuhusiana na uadilifu wa kutoa haki katika vyombo vya haki. Ni muhimu sana na ninaomba suala hili liende moja kwa moja na maboresho ya maslahi ya wafanyakazi au Mahakimu ambao wanahukumu kesi zetu. Tunaona kwamba watumishi wa kada hii ya sheria au Mahakimu ni muhimu wakaboreshewa, hata alivyokuwa anaelezea Mwenyekiti wa Katiba na Sheria ameona kuna tatizo kwamba bado hawajaboreshewa maslahi yao. Sasa inakuwa ni shida sana kutenda haki kama Mahakimu wenyewe. Wanahukumu kesi za mabilioni ya fedha lakini wao wenyewe bado hawana mshahara wa kutosha, pengine bado hata mazingira yao hayako vizuri, ni rahisi sana kuweza kukubaliana kuchukua rushwa na kutotenda haki kwa yule mtu wanayemhukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nielezee kuhusu miundombinu na maboresho katika Mahakama hasa ya Mwanzo. Mahakama za Mwanzo kwa kweli katika sehemu nyingi, hata katika Mkoa wetu wa Iringa zina hali mbaya sana. Mahakama za Mwanzo nyingi wamepangisha au nyingine zina majengo ambayo siyo mazuri. Kwa hiyo, naomba kuwepo na maboresho makubwa katika Mahakama zetu za Mwanzo kwa sababu ndicho chombo cha kwanza ambacho mwananchi anakwenda kudai haki yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakuta Mahakama ina nyufa, hata anaye hukumiwa anaweza akafiri jengo linaweza likambomokea wakati wowote hata bado haki haijatolewa. Kwa hiyo, ni muhimu sana hizi Mahakama zikaboreshwa kwa sababu ndizo Mahakama ambazo mwananchi anakwenda kudai haki yake na ni Mahakama ya Mwanzo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aone umuhimu wa kuja kuboresha hasa Mahakama zetu za Mkoa wa Iringa ambazo nyingi kabisa zipo katika hali mbaya na kwa kweli ni kitu ambacho naomba kizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya niliyozungumza, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili kuwa mchangiaji wa kwanza jioni hii ya leo. Naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuwapongeza Waziri, Mheshimiwa Dkt. Gwajima na Naibu Mawaziri Mheshimiwa, Dkt. Mollel na Mheshimiwa Mwanahamisi. Kwa sababu leo ndiyo siku hii Wizara inayohusika na mambo ya wanawake, naomba kwa kweli nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Kwanza kabisa kwa kuwa Rais ambaye amekuwa akituwakilisha vyema, lakini nimpongeze pia kwa hotuba yake ambayo alikuja kuhutubia hapa Bungeni kuhusiana na mambo ya afya. Ametuhamasisha sana. Vile vile, nampongeza kwa kumteua Naibu Waziri ambaye anashughulika na masuala ya wanawake, wazee na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya masuala siku zote tulikuwa tunaona yanamezwa na masuala ya afya, kwa sababu katika Wizara hii kuna mambo mazito mengi ya wanawake, watoto na wazee ambapo tulikuwa tunaona hata sisi wenyewe tukichangia tunaenda moja kwa moja kwenye afya. Sasa tuna imani Naibu Waziri wetu atachangamsha kuhakikisha kwamba anasikiliza changamoto zinazohusu wanawake, wazee na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais. Amewateua wanawake kwenye nafasi nyeti sana. Kwa hiyo, nampongeza na nina imani kabisa tutawaunga wenzetu mkono na watafanya kazi vizuri akiwemo dada yetu Mheshimiwa Jenista, Mheshimiwa Ummy, Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na wote waliochaguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze hata Wabunge waliochaguliwa katika Majimbo wakiongozwa na wewe mwenyewe. Kwa kweli, tunaona kazi kubwa mnayoifanya na tunawatia moyo na tuna imani kwamba wananchi waone kazi ya mwanamke, wanawake tunaweza na tunasema kwamba mzigo mzito mpe mwanamke, atauweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja sasa kuna vitu viwili nataka kusema. Jamani wanaume mpo? Wanaume mpo? (Kicheko)

WABUNGE FULANI: Tupo.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wale waliosema jamani, hiki ni kipindi cha wanaume sasa kupima UKIMWI. Tulikuwa na Balozi wetu Waziri Mkuu ametuwakilisha vizuri sana kuhakikisha anawahamasisha wanaume kupima, lakini bado hawapimi, wanatupimisha sisi wanawake. Wanaume wengi wanaishi na virusi lakini wanatuficha na wakati mwingine wanameza dawa hawatuelezi, wanaweka sehemu nyingine. Kwa hiyo, niombe kwa kweli kupitia Bunge hili leo hii tuhamasishe wanaume wote wakapime na tuanze na Wabunge wote wanaume muwakilishe wanaume wenzenu kwenye majimbo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu maambuzi mapya ni asilimia 40, utakuta kwamba asilimia 80 ni watoto wa kike. Sasa niseme kwamba unaona kwa watoto wa kike wengi wanaambukizwa kwa sababu pia wanabakwa sana. Watoto wa Iringa, tuna kesi zaidi ya 400 wamebakwa, kuna mwanaume mmoja alibaka watoto saba amewabaka siku moja. Kwa hiyo, kwa kweli niombe kabisa pengine hata sheria ije. Naomba kwa kweli sasa hili liangaliwe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule China watu wakiiba wanauawa, lakini sasa hawa sijui tuangalie adhabu gani maana kitu kinachosababisha watoto wetu wabakwe kiangaliwe vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema kwamba nyumba ni choo. Sasa kulikuwa kuna kampeni ile ya kuhamasisha vyoo bora vijengwe kwenye vijiji vyetu. kunapokuwa na vyoo bora inasaidia kupunguza hata maambukizi yale ya katika maji, kwa sababu bado kwenye vijiji wananchi wanatumia maji ya kwenye mabonde na mito, kwa hiyo unakuta maambukizi yanakuwa mengi sana. Nimwombe Waziri mwenye dhamana ahakikishe kwamba ile kampeni inaendelea kwa sababu bado kuna kaya hazina vyoo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nielezee kuhusu Bima ya Afya. Niombe, naona leo wengi wameongelea kuhusu Bima ya Afya, lakini niombe Bima ya Afya iongeze wigo wa matibabu. Kuna magonjwa ambayo yanawatesa sana wananchi hasa magonjwa ya figo na magonjwa ya saratani. Unaona wananchi wanatumia pesa nyingi sana, wengine ni watumishi tu wa kawaida, wengine hata sio watumishi unaona bima zile bado hazimwezeshi huyu mgonjwa kwenda kutibiwa kwenye hospitali zetu. Wamekuwa wakipata shida, wanakuwa wakienda kule kwenye matibabu inatakiwa watafute nyumba za kupanga. Niombe Serikali yetu hii iangalie wanyonge hawa ambao kwa kweli mara nyingi wamekuwa wakipata mateso makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijikite kwenye changamoto za Mkoa wangu wa Iringa. Jambo la kwanza ni Hospitali yetu ya Mkoa ina shortage kubwa sana ya Madaktari Bingwa kwa magonjwa mbalimbali. Karibu Madaktari saba wanahitajika katika hospitali yetu ya Mkoa wa Iringa. Pia, hii CT scan machine nilishawahi kuleta hata swali ni tatizo kubwa sana kwa wagonjwa wetu pale Mkoani Iringa. Nishukuru kwamba Serikali imesema kwamba itaanza kuleta hizi mashine katika hospitali za rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nielezee changamoto nyingine, ambayo ni upungufu mkubwa sana wa watumishi wa Sekta ya Afya. Unaona karibu asilimia 62 ya mkoani kwetu bado tuna upungufu mkubwa na katika hata baadhi ya Wilaya kwa mfano Kilolo hospitali imeshakuwa tayari kabisa lakini tatizo ni watumishi wa afya. Niiombe Wizara sasa iende sambamba na hizi hospitali zinazojengwa, iweke watumishi ili kuondoa changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hawa watumishi wamekuwa wakifanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Unaona wanafanya kazi kwenye maeneo hatarishi, hata wakati wa covid vifaa havikuwepo vya kutosha. Kuna wengine walipoteza maisha. Naomba pia Serikali iangalie pia na suala la vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusiana na dawa MSD. Kuna malalamiko kwamba watu hawapati dawa wanalazwa lakini dawa hawapati. Inabidi tena waende wakatafute sehemu nyingine. Mimi niombe kwamba MSD ijitahidi kwa sababu ilibidi nifanye ziara kwenye hii Hospitali ya Mkoa na wakasema kwamba wanapeleka asilimia 50 ya yale makusanyo lakini dawa wanazohitaji kule hakuna. Sasa iwe kama zamani kwamba kama hakuna dawa basi waangalie labda kwa wale washitiri, kwa maana waruhusiwe kwenda kununua hizo dawa, kwa sababu limekuwa ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nitoe pongezi kubwa sana. Tumekuwa na watu ambao wanachangia Wizara yetu ya Afya lakini bado sijajua kama Serikali inawatambuaje. Kwa mfano, kwenye Mkoa wetu wa Iringa tunayo majengo ambayo yamejengwa na wadau wa maendeleo. Kwa mfano, nimpongeze Mheshimiwa ASAS, labda nitaje tu baadhi ya majengo ambayo amejenga. Kuna jengo la Benki ya Damu, Wodi ya Watoto Njiti na vifaa vyake, ICU unit, Jengo la Kiwanda cha Viungo Bandia, jingo la Kituo cha Ustawi wa Jamii na mengine mengi. Kwa kweli, naomba tutambue michango ya wadau ambao wamekuwa wakisaidia hata bajeti yetu ya Wizara ya Afya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele imegonga.

MHE. DKT. RITTA E. KAKABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hii hoja muhimu. Kwanza nianze na kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na Katibu Mkuu, Mr. Kijazi na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya na kutuletea bajeti hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na mradi wa REGROW. Mradi huu ni mradi wa kukuza utalii Kusini. Huu mradi kwa kweli, umeanza mwaka 2018 na tunategemea mwaka 2023 utakuwa umekamilika, lakini naona kama kasi ya mradi huu ni ndogo sana. Kwa sababu, huu mradi tunategemea sasa Nyanda za Juu Kusini tuna vivutio vingi, Wabunge wengi sana wa Nyanda za Juu Kusini wameongea vivutio vyao vilivyopo katika mikoa yao. Hata hivyo, kama huu mradu utakuwa haujakamilika bado tutakuwa hatujawasaidia wananchi wa Nyanda za Juu Kusini kupitia Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitegemea kwamba huu mradi ungeleta ajira nyingi za vijana, akinamama na watu wote na ungeongeza pato kubwa sana, lakini hatuelewi kama mwaka 2023, huu mradi utakuwa umeshakamilika au umeshaanza kufanya kazi yake. Kwa sababu Makao Makuu ya huu mradi yanategemea kuwepo Iringa lakini pia GN ndiyo kwanza juzi tu tumeona imesainiwa na yenyewe ilichukua muda mrefu sana kusainiwa. Pia bado hatujaona hata Makao Makuu yenyewe yameshaanza kujengwa na tunategemea sasa kutakuwa na vyuo vingi pale Iringa kwa ajili ya Nyanda za Juu Kusini, Vyuo vya Misitu, Maliasili na kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali ilichukue suala hili kwa umuhimu wake ili kuhakikisha kwamba huu mradi unakamilika na unaleta manufaa. Ikiwezekana labda kuwepo na mashindano kati ya Nyanda za Juu Kusini na Kaskazini, pengine labda hata watendaji wangechamka kuona kwamba haya mashindano yanaleta manufaa na pengine tungekuwa tunawapatia zawadi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia vivutio bado havijatangazika kiasi cha kutosha. Bado tunaweza tukawa na utalii wa ndani kama vivutio vyetu itakuwa watu wanavielewa na nafikiri Wabunge wengi sana wamezungumzia kwamba utalii wa ndani pia unaweza ukalipa, unaweza ukasaidia pia hata mafunzo kwa watoto wetu, wakue wakijua kwamba tuna utalii katika nchi yetu. Hiyo inaweza ikamjenga kwamba sisi tuna maliasili ambazo zinaweza zikatusaidia wananchi wote. Kwa hiyo, niombe kwa kweli matangazo yaongezeke, biashara ni matangazo. Matangazo yakiwa mengi, vivutio vyetu vitaeleweka na wananchi watakwenda hata kuviangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nielezee kuhusu Ruaha National Park. Kwa kweli, hii mbuga ni ya pili kwa ukubwa na niliona hata Mwenyekiti wa Kamati aliizungumzia kwamba hii mbuga imesahaulika wakati ina wanyama wazuri, ina wanyama wengi, barabara haifikiki kabisa. Maana hii ingesaidia hata utalii wa ndani kama barabara ingekuwa inafikika. Hata sisi wenyewe Wabunge, nishukuru kwamba Kamati ilikwenda kutembelea na imeona changamoto nyingi sana zilizopo katika Ruaha National Park. Kwa hiyo, niombe kwa kweli ile barabara Waziri wa Ujenzi na Mawaziri wote wapiganie, watoe kipaumbele kwa hii barabara kwa sababu ni barabara ambayo itasaidia kabisa kukuza utalii katika nchi yetu na kuleta pato kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie kuhusiana na utalii ulioko Iringa Manispaa. Kuna sehemu ambapo wakoloni walikuwa wananyongea watu, panaitwa kitanzini. Pale kuna kitanzi ambacho kuna boma lake limebomoka kabisa, yaani watalii wanatakiwa waje watembelee. Nitamwomba hata Mheshimiwa Naibu Waziri Masanja twende sio mbali sana, akaone jinsi ilivyo. Pamesahaulika kabisa wakati ni utalii mzuri. Kuna jiwe lile Gangilonga, lilikuwa linaongea zamani, hata watalii wakienda…kutembelea pale wanapata madhara wanavamiwa. Kwa hiyo, ni vizuri hivi vivutio vingewekewa mkakati kwanza viwe vinafikika na viwe vinatangazika, lakini tatizo kubwa kwenye halmashauri zetu hakuna Maafisa Utalii. Kwa hiyo, unakuta kwamba, kuna Maafisa Kilimo, kuna afisa nani, lakini Afisa Utalii bado Wizara haijawapa kipaumbele, hakuna connection kabisa, unaona wanajifanyia tu kazi wenyewe, hawana vifaa, hawafanyi kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ingewezekana pengine labda Wizara itoe ruzuku kwenye halmashauri, ili hivi vivutio viweze kufikika na viweze kutangazika vizuri ili tuweze kuongeza pato kubwa sana katika halmashauri au kuwepo na kurugenzi inayoshughulikia mambo ya utalii tu katika manispaa zetu kwa sababu ndiko kwenye utalii mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kuhusu mazao ya misitu. Tunayo mazao ya misitu Mufindi, Kilolo na kwingine kwingi Njombe, lakini tunaona tozo zimekuwa nyingi sana, karibu tozo 13 kwenye mazao ya misitu. Wananchi wengi wengine wamepanda haya mazao ili yawasaidie kusomesha watoto, yawasaidie kama ajira pia, lakini tozo zikiwa nyingi bado tunaona hatujamsaidia Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nikushukuru, lakini niombe kwamba, matangazo, Simba niwapongeze kwamba, wametangaza nchi kwa kutumia jezi zao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya, kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana na naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia jioni hii ya leo. Kwanza kabisa, nami niungane na wengine wote ambao wametoa pongezi nyingi sana kwa mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu, Rais wetu ambaye kwa kweli amefanya mambo mengi sana makubwa na mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna usemi unasema kwamba mzigo mzito umpe Mnyamwezi, lakini kwa kazi nzuri mama anayoifanya, inaonesha kwamba sasa tubadilike, tuseme kwamba mzigo mzito mpe mwanamke na wanawake tumekuwa tukibeba mizigo mizito sana na ninyi akina baba mnajua kwamba mizigo mizito huwa haitushindi. Tuna imani kabisa mama hatashindwa. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitoe pongezi...

MWENYEKITI: Nilisikia kuna taarifa upande huu. Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, endelea na mchango wako. (Makofi/Kicheko)

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawe ni lazima uunge mkono kwamba wanawake huwa hatushindwi, mizigo mizito yote huwa tunaiweza. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na Naibu wake na Watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea Mpango ili tuweze kuujadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitakuwa sijatenda haki kama nisipompongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Bajeti Mheshimiwa Dkt. Sillo na Wajumbe wote wa Kamati ya Bajeti, kwa kweli wametufafanulia vizuri sana huu Mpango na ndiyo maana tumeweza kuuchangia vizuri. Nawapongeza sana kwa kazi nzuri, wala hawakufanya kosa kuwachagua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwa kweli niungane na wote, nianze mchango wangu kwa kuchangia Sekta ya Kilimo. Sekta ya Kilimo kama ambavyo imesemwa kwamba Watanzania zaidi ya asilimia 65 ni wakulima. Vilevile Sekta ya Kilimo inatoa ajira karibu asilimia 66.3; pia inachangia katika viwanda asilimia 60; na pato la Taifa ni asilimia 26. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Wajumbe wote kwamba bado kabisa Wizara ya Kilimo haijaweza kupewa kipaumbele cha kutosha. Bajeti ya Wizara ya Kilimo ni ndogo sana. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kilimo. Siku zote tumekuwa tukilalamikia Bajeti ya Wizara ya Kilimo.

Tunao Mawaziri wazuri sana tu katika Wizara ya Kilimo; ni wazuri sana kwa sababu tunafanya nao kazi, lakini katika Kamati yetu ya Kilimo tunao wabobezi wazuri sana. Tuna Wajumbe wazuri ambao siku zote wamekuwa wakitoa michango yao, tumekuwa tukitoa michango yetu pale, tumekuwa tukitoa hoja zetu, tumetoa ushauri mzuri kuhakikisha kwamba kilimo chetu kiwe na tija, lakini je, hii michango, huu ushauri unachukuliwa wakati gani na kufanyiwa kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tumeona Mpango umekuja, lakini mambo mazuri ambayo tumeishauri Serikali yetu, bado hatujaona kama yamechukuliwa katika huu Mpango. Sasa nilikuwa naomba kuwepo basi na mkakati tuone yale tuliyoyashauri yamefanyiwa kazi kiasi gani? Yametekeleza kiasi gani? Kwa nini hayatekelezeki? Nini tufanye ili tuwe na mipango mizuri kuhakikisha kwamba kilimo kinaweza kuisaidia nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima nchini kwa kweli wamekuwa wakilima tu kilimo cha mazoea. Wakulima wetu wanalia, wakulima wetu wamekuwa wanafanya kazi kubwa, lakini hamna wanachokipata. Watu wanajuta hata kuwa wakulima. Ili kilimo chetu sasa kiwe na tija, tunahitaji tuwe na Mpango mzuri. Tuhakikishe tunakuwa na Maafisa Ugani. Tunaona wakulima wengi wanalima bila kuwa na elimu ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda mkoa wetu wa Iringa unaona hata kusafisha mashamba wanachoma. Leo Iringa wanalia, misitu imeungua; ukienda Kilolo au Mufindi, sasa hivi tumeunguza mashamba mengi kwa sababu wakulima hawana elimu ya kutosha kuhakikisha kwamba wanasafisha hata mashamba tu kwa utaalamu. Vilevile wanalima kilimo ambacho hakina tija kwa sababu wanafundishana wao wenyewe. Kuna shortage kubwa sana ya Maafisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuwepo na ruzuku katika pembejeo. Ukifanya ziara sasa hivi tatizo kubwa ni bei kubwa ya mbolea. Wananchi sasa hivi wameanza kuandaa mashamba, bado mbolea iko bei juu sana, hawajui wafanye nini. Naomba ruzuku ya pembejeo ni muhimu sana tupate mbolea, bei iwe chini, lakini pia hata mbegu bora ziwe bei ya chini kabisa ili wakulima wetu waweze kulima kilimo chenye uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuwepo na uzalishaji wa mbegu bora, lakini vilevile masoko ni tatizo kubwa sana kwenye nchi yetu. Wakulima wanalima mazao mengi lakini hawana uhakika wa soko la kesho litakuwaje, wanakuwa wanalima kwa hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba vilevile ujenzi wa vihenge pamoja na maghala, ni muhimu sana. Sasa hivi wakulima wengi hawana sehemu za kuhifadhia mazao yao, changamoto ni hiyo sasa mazao hayo yanashambuliwa na wadudu. Tumpongeze sana Mheshimiwa Rais, alikuwa ametoa zile bilioni 100 kwa ajili ya soko la mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, unaona kutokana na kutokuwa na maghala sehemu ambayo wakulima wapo wameshindwa kwenda kuuza yale mahindi kwa sababu ukiangalia gharama ya kupeleka yale mahindi sehemu ya kununulia yale mazao, ni mbali na ni ghali, kiasi kwamba bado hawajafaidika, waliofaidika ni madalali ambao wao wanachukua mahindi wanayapeleka kwenda kuyauza kule kunakotakiwa kununuliwa yale mahindi. Kwa hiyo niombe maghala ikiwezekana yawepo kila kata ili kusaidia wakulima kupata urahisi wa kuhifadhi mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, wakulima hawakopesheki benki; benki zetu haziwakopeshi wakulima. Kwa sababu tunayo Benki ya Kilimo tulitegemea sasa hii benki ingekuwa msaada kwa wakulima, wangepewa ruzuku ya kutosha ili wakulima wakope kwa riba nafuu, lakini benki hii bado hatujajua sasa imekuja kumsaidia mkulima au imekuja kufanya biashara, kwa sababu bado riba iko juu sana. Kwa hiyo, naomba uwepo mpango mkakati kuhakikisha wakulima wetu wanakopesheka ili waweze kulima kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie kuhusu jitihada ya Serikali kulipa madeni ya wazabuni, lakini vilevile hata wazabuni wa pembejeo wengi bado wanadai. Nilitegemea hawa wazabuni wangelipwa kwa wakati ili waweze kuleta sasa hizo pembejeo kwa wakati na ziweze kufikia wakulima kwa wakati. Hata hivyo, wazabuni mpaka leo hii bado wanadai madeni makubwa, wanashindwa kwenda kununua hizo pembejeo, kuwasogezea wakulima ili waweze kulima kwa wakati. Misimu inakuja bado ukienda kuwaona wale wa pembejeo wanasema bado wanadai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uwepo mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba wazabuni hawa wanalipwa. Wengi wao wamechukua mikopo benki, wengi wao wanatishiwa kuuziwa mpaka mali zao. Sasa naomba kwa kweli wazabuni wa pembejeo wapatiwe pesa zao kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mfano kuhusiana na mkulima wa nyanya, kwa sababu hata mimi ni mkulima wa nyanya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa na mimi nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo Mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu. Pia, niwatakie Ramadhan Karim Waislam wote pamoja na Wakristo wote ambao wamefunga katika mwezi huu Mtukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na wote ambao wameweza kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambazo amekuwa akizifanya na hotuba yake, vilevile niendelee kuwapongeza wote waliompongeza Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia. Kwa kweli anafanya kazi nzuri na anatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa vitendo. Naomba Watanzania wote hasa akina Mama na akina Baba tumuunge mkono ili kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze hoja yangu kwa kuzungumzia jambo kubwa lililopo katika Mkoa wetu wa Iringa, kuhusiana na ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto. Hili ni janga la Taifa. Tulipopokea taarifa katika RC tuliona karibu matokeo 439 kwenye Mkoa wetu yameripotiwa ya ukatili wa kijinsia. Kuna Wabunge wamechangia kuhusiana na huu ukatili, hili jambo ni zito mno. Mimi naomba Serikali iangalie, hili ni tatizo kubwa ambalo tunatakiwa tuungane na tunatakiwa sasa tuanze kulifanyia kazi na itengwe bajeti kuhakikisha kwamba hili janga katika Tanzania tunaanza kulitatua ili tutengeneze watoto ambao watakuwa kizazi kizuri katika nchi yetu. Hili ni tatizo kubwa ambalo tunatakiwa tuungane na tunatakiwa sasa tuanze kulifanyia kazi na itengwe bajeti kuhakikisha kwamba, hili janga katika Tanzania yetu tunaanza kulitatua ili tutengeneze Watoto ambao watakuwa kizazi kizuri katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ambayo niliyabaini nilipofanya ziara katika Mkoa wa Iringa na Wilaya zake zote. Sasa hivi kwanza watoto wameanza kubakana wao kwa wao, wanalawitiana wao kwa wao. Tatizo kubwa ambalo lipo hasa watoto wadogo ambao wanasoma Shule za Msingi, unakuta kwamba shule zetu nyingi za msingi hazikarabatiwi, hazina vyoo, hazina uzio kwa hiyo, unakuta watoto wanashindwa kwenda chooni wanakwenda kuomba kwa majirani, wanakwenda kwenye milima kujisaidia wao kwa wao kwa hiyo, huko ndiko ambako wanabakana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeshaona kwenye vyombo vya Habari sasa hivi tunaona kwamba, karibu kila Mkoa hili janga lipo. Kwa hiyo, naiomba Serikali hebu tutenge bajeti ya kutosha tuhakikishe shule zetu za msingi zinakuwa na vyoo, shule zetu za msingi zinakuwa na uzio kulinda hawa watoto wetu ambao sasa hivi hili limekuwa ni janga kubwa ambalo linahitaji maombi hata viongozi wa dini sasa hivi watusaidie pengine ni pepo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo nilikuwa nataka kulizungumza, nilitaka kuzungumza taharuki ambayo imejitokeza katika Mkoa wetu wa Iringa na Njombe. Tunaona Mheshimiwa Chumi alizungumza kuhusiana na TANESCO kuanza kuagiza nguzo kutoka nje, leo hii tumemuona Mbunge wa Njombe Mjini na yeye ameielezea hiyo taharuki na mimi kama Mbunge wa Iringa katika hiyo Mikoa miwili, niombe kwanza kabla sijazungumza kwamba Waziri mwenye dhamana hebu akae na Wabunge, Waziri mwenye dhamana ikiwezekana hata tuende tukafanye mikutano mikubwa kwenye Mikoa yetu ya Iringa na Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu ulikuja Iringa, ulishuhudia wewe mwenyewe ulifungua nembo yetu, ile Iringa Woodland, kama ambavyo labda wenzetu Mwanza wana Rock City sisi tuna Woodland. Kwamba, Mkoa wetu wa Iringa kipato kikubwa kinatokana na mazao ya misitu. Sasa hivi Halmashauri zetu nyingi zinategemea misitu na tuna viwanda zaidi ya 18 kwenye Mikoa hii miwili, kuna ajira nyingi sana imetengenezwa kupitia nguzo. Sasa tunaomba Mheshimiwa Waziri Mkuu hebu uangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mapato ya Halmashauri kwa sababu, hizi asilimia 10 unaona akina Mama, Vijana na Watu Wenye Ulemavu walipata mikopo mikubwa hata Mheshimiwa Ummy alivyokuja pale Iringa kutokana na mapato makubwa yaliyopatikana kutokana na mazao ya misitu ambayo ni nguzo. Kwa hiyo, tunaomba kabisa hili jambo lisipuuziwe tukahikishe kwamba, tunakaa ili kutatua hili tatizo ili Mikoa hii iendelee kutumia misitu au hizi nguzo. Kama kuna changamoto kwa nini Wizara ya Viwanda isilete ile teknolojia ikafundisha katika viwanda vyetu ili nguzo ziwe na kiwango? (Makofi)

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Kuna Taarifa wapi? Aah! Mheshimiwa Neema Mgaya, taarifa.

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Ritta kwamba, kinachosikitisha zaidi nguzo hizo hizo ambazo zinatoka Njombe na Iringa na maeneo mengine ya Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, zinatoka tu nje ya Tanzania zinakwenda zinarudi tena kwa mlango mwingine zije kuuzwa kwa bei kubwa, wakati nguzo ni za kwetu wenyewe Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Mheshimiwa Ritta napenda kukwambia kwamba, Mheshimiwa Waziri kuna haja ya kukaa na Wabunge wa Nyanda za Juu Kusini, hususan Wabunge wa Mkoa wa Iringa na Njombe ambao tunalima mbao hizi na kutengeneza nguzo hizi ili kuweza kuisaidia Tanzania kutotumia gharama kubwa katika gharama za nguzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile…

MWENYEKITI: Ahsante kwa taarifa Mheshimiwa Neema Mgaya. Mheshimiwa Ritta Kabati unapokea taarifa?

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naipokea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ndiyo kweli kabisa. Isitoshe TFS inazalisha nguzo kwa kiwango kikubwa sana, sasa na yenyewe itakosa mapato kwa sababu ni taasisi pia ya Serikali, vilevile wanawake, vijana na wananchi wa Iringa wamehamasika kwa kiwango kikubwa kuhakikisha kwamba wanalima miti ya kutosha katika Mkoa wetu wa Iringa. Hiki ndiyo kipato chetu na sisi kama ambavyo wengine wanasema kuhusu korosho, wengine wanazungumza kuhusu makinikia, nasi makinikia ya Mkoa wa Iringa ni misitu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nguzo zetu hazina kiwango ndiyo hivyo nimesema kwamba, Wizara ya Viwanda ilete hiyo teknolojia ili tuzalishe nguzo zenye viwango ili tuweze kupata pato kubwa katika kutumia misitu yetu. TBS wapo na wenyewe waangalie wanatumia teknolojia gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni kuhusiana na hizi asilimia 10 ambazo zinatolewa katika Halmashauri zetu ambazo wanapewa Vijana asilimia Nne, akina Mama asilimia Nne, na Watu Wenye Ulemavu asilimia Mbili. Mimi naiomba Serikali waboreshe hii mikopo badala ya kupatiwa pesa unaona katika taarifa vijana wengi sana bado kuna pesa ambazo hawajazichukua, ni kwa nini Serikali isianze kutoa vifaa au mashine ili tuwe na viwanda vidogovidogo katika Halmashauri zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano labda kwa vijana. Vijana ambao wamesomea wanaweza wakapewa mashine za kufyatua tofali na wameshajifunza na hapohapo Halmashauri ile ikaweza kuchukua tofali kwa vijana wetu. Mimi naomba kwa kweli, jambo hili liangaliwe na nitaliandika kwa vizuri zaidi ili hii mikopo ya akina mama, vijana na wanawake iweze kuwasaidia vijana, iweze kurudi iwe revolving fund. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba niunge mkono hoja, niseme tuungane wote kuhakikisha tunamsaidia Mama yetu Rais, ili kazi iendelee. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia jioni hii ya leo. Nami nianze kwanza kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati ya Miundombinu, Mwenyekiti wa Kamati ya Maji, Kilimo na Mifugo kwa taarifa zao nzuri ambazo wameziwasilisha hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nami ni Mjumbe wa Kamati ya Maji, Kilimo na Mifugo. Niungane na wajumbe wenzangu kwanza kukubaliana na hoja ambazo zimeletwa na Kamati.

Mheshimiwa Spika, tumeweza kutembelea miradi mingi sana iliyopo katika kamati yetu. Miradi mingi tumekuta kuna baadhi ya changamoto ambazo ziko katika miradi ya maji. Kwa mfano tulienda katika mradi ule wa maji wa Mwanza. Tulikuta Serikali inajitahidi kupeleka fedha lakini fedha zinakuwa hazipelekwi kwa wakati. Kwa hiyo, changamoto yake tunakuta kwamba miradi haikamiliki kwa wakati lakini pia miradi inapokamilika inaongezeka gharama zake kwa sababu kwanza kabisa wale wakandarasi msipopeleka fedha kwa wakati kunakuwepo na penalty katika ile miradi. Kwa hiyo, tunajikuta kwamba miradi mikubwa tunatekeleza kwa gharama kubwa sana. Kwa hiyo, nilikuwa ninaiomba Serikali katika hii miradi ambayo inatekelezwa mikubwa hasa ya maji, fedha zipelekwe kwa wakati ili hii miradi iweze kutekelezwa kwa wakati na kusiwepo na ongezeko.

Mheshimiwa Spika, vilevile niendelee kuchangia kuhusiana na Wizara ya Maji, nilikuwa naomba tuwe na Sera ya Uvunaji Maji ya Mvua kwa sababu kumekuwa na mvua nyingi sana katika nchi yetu kwa baadhi ya mikoa ambazo hizi mvua sasa zinasababisha hata mafuriko, zinasababisha uharibifu mkubwa sana wa barabara zetu hasa za vijijini. Kwa hiyo, kukiwepo na Sera ya Uvunaji Maji maana yake maji yatakwenda kwenye ile mikondo au watatengenezewa mabwawa makubwa ambayo baadae sasa yatakuja kufaidisha kwamba yatasaidia hata umwagiliaji katika miradi ya kilimo lakini vile vile yatasaidia hata bajeti ya barabara za vijijini zitapungua.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tumekuta kwamba barabara nyingi za vijijini zinaharibika kutokana na mafuriko ambayo yanasababisha barabara nyingi kuharibika kutopitika wakati wa mvua, lakini barabara nyingi na madaraja mengi yanasombwa wakati wa mafuriko yale ya maji, kwa hiyo, sasa kama tutakuwa na sera ya uvunaji maji ya mvua utasaidia sana hata bajeti ya utengenezaji wa barabara ambazo zinakwenda katika vijiji vyetu. Kwa hiyo, miundombinu itakuwa mizuri kwa sababu wananchi wataweza kupata maji kwa wakati na vilevile tutaweza kufaidika kwamba barabara nyingi hazitatengenezwa kila wakati.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nizungumzie kuhusiana na kilimo cha mboga mboga na matunda. Serikali niipongeze imeweza kuhamasisha sana kilimo cha matunda na mboga mboga na hasa hata hizi parachichi. Nilikuwa naomba tulivyotembelea tumekuta kuna changamoto nyingi sana kwamba kamati yetu ilikuwa inaomba sasa Serikali ifanye miundombinu kuwepo na miundombinu kwa ajili ya usafirishaji wa haya mazao katika airport zetu na katika bandari zetu. Vilevile itenge eneo maalum la green belt katika bandari zetu ili iweze kusafirishwa kwa uhakika. Tumeona kwamba nchi kama Kenya wanakuja kuchukua kwa mfano parachichi kupeleka kwenye nchi zao na matokeo yake sasa wao kwa sababu wana miundombinu rafiki katika airport zao wana miundombinu rafiki katika bandari zao, unakuta hata parachichi zetu wanazichukua na kwenda kuona kwamba wao ndiyo wanaozisafirisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe pia Serikali hiyo logistic za usafirishaji hata barabarani unakuta bado haya mazao yakisafirishwa askari wanayasimamisha kiasi kwamba hakuna logistic nzuri za kusafirisha haya mazao.

Mheshimiwa Spika, vilevile tulivyotembelea katika baadhi ya taasisi tumekuta kuna changamoto ya wafanyakazi. Hawa wafanyakazi wamekuwa wakipata mikataba ya kufanya kazi katika taasisi hizo, mfano tulivyotembelea shamba la ASA kule Arusha, tumekuta wafanyakazi wanapewa mikataba kufanya kazi katika hayo mashamba lakini linapokuja suala la ajira unakuta wale wafanyakazi ambao tayari wameweza kujengewa uwezo mkubwa unakuta ajira ikija hawaajiriwi. Kwa hiyo, Serikali inaajiri wafanyakazi wapya kabisa kiasi Serikali inakuwa haifanyi vizuri sana, wanakuwa wanaanza upya kuwafundisha.

Mheshimiwa Spika, pengine sasa uwepo mkakati wale wafanyakazi ambao tayari wamepewa mikataba na wana uwezo wa kufanya ile kazi wapewe kipaumbele cha kuendeleza ule mradi ili isiwepo wakati wa ajira, wale ambao tayari wameshafanya pengine miaka miwili au mitatu hawapatiwi ajira, hilo lingeangaliwa.

Mheshimiwa Spika, pia nipongeze kazi nzuri ambayo inafanywa na Wizara ya Maji na Wizara ya Kilimo katika miradi ambayo tumeipitia. Kwa mfano tulikwenda kwenye miradi ya Dar es Salaam tumekuta kwa kweli kulikuwa kuna upungufu mkubwa hakuna mtu ambaye hakai Dar es Salaam. Changamoto zilikuwa nyingi sana. Pia wana changamoto ya wafanyakazi. Unakuta kwamba wafanyakazi wengi wanapewa mikataba lakini wakati wa ajira bado unaona wana uwezo wa kuwalipa wale vijana lakini Serikali inachelewesha zile ajira kiasi kwamba sasa wangekuwa pengine wangeweza kukusanya mapato mengi sana lakini wanakuwa mapato yale hayakusanyiki kwa sababu ya uhaba wa wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pengine hilo nalo lingepewa kipaumbele hizi mamlaka zenye uwezo wa kuajiri vijana basi waweze kuajiriwa kwa wakati ili waweze kufanya kazi ambayo watakusanya mapato kwa wakati.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili Mheshimiwa.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ninaunga mkono hoja zote.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani. Mimi pia nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi wanayoifanya, lakini kutuletea bajeti hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Iringa zaidi ya asilimia 50 ni wanawake, tukianza na RC ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, lakini pia tunaye Kamanda wa Zimamoto, tunaye Kamanda wa Uhamiaji pamoja na TAKUKURU. Naomba Wizara ilete pesa nyingi sana katika Mkoa wetu wa Iringa ili wanawake hawa waweze kufanya kazi wanajituma sana pasipo kuwa na hakuna fedha za kutosha katika mkoa wetu. Kwa hiyo, naomba waletewe pesa ya kutosha ili kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo wenzangu wamesema, askari wetu wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana, hasa katika Mkoa wetu wa Iringa. Hakuna kitu kinachokatiza, wahamiaji haramu wamekuwa wakikamatwa kwa wingi sana kwenye Mkoa wetu wa Iringa. Kwa hiyo ninaomba; changamoto ya nyumba za polisi kila mkoa ipo ukiwepo Mkoa wetu wa Iringa. Askari anatoka katika lindo anarudi nyumbani anashindwa hata kufanya mambo mengine kwa sababu, kwanza anakaa chumba kimoja na watoto na isitoshe nikichukulia mfano hata katika pale FFU Kihesa, mimi nimezaliwa pale, tangu nimezaliwa zile nyumba hazijawahi kufanyiwa ukarabati, unakuta hakuna vyoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawahurumia sana akinamama na watoto wanaoishi katika maeneo ya makazi ya askari. Kwa kweli ninaomba kabisa Serikali iwe na mkakati maalum wa kuhakikisha kwamba, hizi nyumba za askari zinajengwa tena ni kwa majeshi yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija katika Wilaya ya Kilolo unakuta miaka 20 katika makao makuu hakuna ofisi ya OCD. OCD anakaa TAZAMA Pipeline, DC yuko kwenye makao makuu. Wale mahabusu wanakaa TAZAMA Pipeline na hakuna gari la kuwapeleka yaliko makao makuu. Kwa hiyo, mimi naomba Wilaya ya Kilolo iangaliwe kwa karibu kwa sababu, kwanza kabisa wana eneo kwa ajili ya kujenga makao makuu ambalo bado halijalipiwa hata fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo ile Barabara ya Kitonga. Unakuta kila wakati ile barabara inakwama kwa sababu ya ajali nyingi. Kwahiyo, itatakiwa usalama, na hivyo lile eneo linatakiwa kuwa na kituo cha polisi kitakachokuwa karibu. Hii ni kwa sababu, ndani ya siku mbili ama tatu katika ile barabara kunatokea ajali. Jambo lingine kuna shortage pia ya askari polisi. Kwa hiyo, tunaomba askari polisi kwa wingi Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie kuhusu Jeshi la Magereza. Jeshi la Magereza changamoto zao kwanza ni makazi kama walivyo askari wengine, lakini pia naomba Jeshi la Magereza lichukuliwe kama jeshi la mafunzo, ni kituo cha mafunzo. Wale watu walioko pale wafundishwe, wapatiwe mikopo ili wanapotoka watoke na elimu lakini pia wapatiwe pesa ili wakaanze kuendeleza kile walichokipata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile kuna tatizo la matrekta. Wanafanya kilimo kizuri sana lakini matrekta yao yote ni mabovu. Tunaomba pia waongezewe matrekta ili waweze kujikimu kwa chakula na waweze kujitunza wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tatizo jingine ni kwamba, wanatakiwa wapatiwe mablanketi na masweta. Mkoa wetu wa Iringa una tatizo kubwa sana la baridi, kwa hiyo unakuta wafungwa wanapata pneumonia na wana zahanati pale ambayo haina ruzuku kwa hiyo sasa hawana bima ya afya. Sasa tunaomba kile kituo kwanza kipewe ruzuku ili waweze kutibiwa pale katika Zahanati ya Magereza ambayo inatibu hata raia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunalo gereza letu ambalo liko pale Mgagao. Hili Gereza la Kihesa Mgagao unaona kwamba…

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Nusrat Hanje.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, mzungumzaji anayezungumza nakubaliananaye na ninaomba nimpe Taarifa tu kwamba, anachokiongea ni very valid, ni cha halali kwa sababu, wafungwa hawaruhusiwi kabisa kutumia nguo yoyote ya uraiani hata ya kujifunika kujisitiri na baridi. Kwa hiyo, suala la mavazi ya kujisitiri kwenye baridi kama mablanketi na masweta na mavazi yao kwa ujumla ni muhimu sana, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa sababu, ndilo tatizo kubwa lililopo hata katika Gereza letu la Iringa na magereza nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunalo Gereza la Kihesa Mgagao, Wilaya ya Kilolo. Tunaomba Serikali sasa ifanye utaratibu aidha, ilihamishe lile gereza au ibadilishe matumizi. Kwa sababu, naona lile gereza lilikuwa kama lilivyo, kuna maeneo ambayo waliishi wakimbizi wa Kusini mwa Afrika ambako maeneo yote unaona kwamba, wameweka kumbukumbu. Kwa mfano ukiangalia Mazimbu kuna campus ile ya SUA, lakini ukiangalia pia Dakawa kuna shule, kuna chuo, lakini pia ukiangalia pale Kongwa sasa hivi kuna kituo cha Ukombozi wa Afrika, kimetoka makao makuu. Sasa kwa nini Kilolo hilo gereza tusiende kujenga kwingine ili pale kuwe kuna kumbukumbu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kuna vyumba ambavyo alilala Nelson Mandela, kuna vyumba ambavyo walilala marais wengi waliokuja kupigania uhuru. Kwa hiyo, ninaomba kabisa kiwe kama kivutio na ikiwezekana sasa pale watu wawe wanakuja kuangalia iwe kama utalii kuliko ilivyo sasa hivi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. Kengele imeshagonga.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga hoja mkono, lakini niliandika kwa maandishi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kuwapongeza Waziri Mheshimiwa Masauni, Naibu Waziri Mheshimiwa Jumanne Sagini, pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea hotuba ya bajeti ili tuweze kuijadili na kuishauri Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, nitaanza na mambo yafuatayo; kwanza ni uhusu Jeshi la Polisi; changamoto kubwa ni uchakavu mkubwa wa makazi na upungufu mkubwa. Katika Wilaya ya Kilolo hawana kabisa nyumba za askari wala ofisi ya OCD yalipo Makao Makuu ya Wilaya karibu miaka 20 sasa.

Mheshimiwa Spika, kuna ofisi za Serikali zinatumika kama kituo cha polisi. Eneo lipo lakini halijalipiwa fidia. Sasa tunaomba Serikali itoe pesa ya kutosha kwa Mkoa wa Iringa ili kazi za Jeshi la Polisi ziendelee.

Mheshimiwa Spika, kituo cha polisi Ruaha Mbuyuni ni kituo mtambuka, kinahudumia Jimbo la Mikumi na Jimbo la Kilolo, lakini hakina gari (eneo kutoka kituo kikuu ni mbali sana). Pia Kituo cha Polisi Kitonga ni muhimu sana na kinahitajika kutokana na ajali za mara kwa mara na ulinzi wa abiria na mali zao.

Mheshimiwa Spika, jeshi hili lina upungufu mkubwa wa askari kwa sababu kuna kesi nyingi za mauaji na ubakaji upelelezi unachukua muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, kwa Jeshi la Zimamoto tunashukuru sasa hivi Kamanda ana usafiri pongezi, lakini jeshi hili halina magari ya kutosha ya kuzimia moto, yaliyopo ni machakavu sana.

Mheshimiwa Spika, katika mkoa wetu tunayo misitu ya mazao ya mbao katika Wilaya ya Mufindi na Kilolo na kumekuwa na matukio ya mioto mara kwa mara, lakini sasa hivi Serikali imejenga shule, mabweni pia tunasambaza umeme vijijini kwa hiyo magari ya uokozi ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, pia tunayo barabara ya Kitonga ambayo mara nyingi kumekuwa na ajali za mara kwa mara na kusababisha barabara kutopitika karibu siku nzima, hivyo muhimu jeshi hili kupatiwa gari la uokozi (crane).

Mheshimiwa Spika, jeshi hili lina uhitaji mkubwa wa nyumba na askari. Pia wana viwanja tayari katika Wilaya ya Kilolo na Mufindi lakini pesa ya ujenzi inahitajika.

Kwa upande wa Jeshi la Uhamiaji; Jeshi hili lina changamoto ya kutokuwa na magari katika Ofisi za Wilaya ya Kilolo na Mufindi. Nyumba za watumishi pia wana viwanja Wilaya ya Mufindi lakini hawana pesa. Wana madeni mengi na magari mabovu. Waongezewe OC na wapatiwe kwa muda unaotakiwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Jeshi la Magereza; changamoto kubwa ya Jeshi hili ni makazi ya askari, msongamano wa mahabusu unaotokana na wahamiaji haramu, wanahitaji vitendea kazi vya kilimo kama matrekta ni machakavu, Mkoa wa Iringa ni baridi kali, wafungwa wanahitaji masweta mazito na mablanketi, wanapata nimonia na hawana bima za afya na pia wana zahanati lakini hakuna ruzuku ya Serikali ya kusikia pamoja na kusaidia raia.

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Serikali ibadilishe matumizi ya Gereza la Kihesa Mgagao lililopo Wilaya ya Kilolo, Mkoa wa Iringa kwa sababu maeneo yote waliyokaa wapigania uhuru wa Kusini mwa Afrika ikiwemo nchi za Afrika ya Kusini, Msumbiji na Angola katika mikoa yote wamejenga vyuo vikuu na shule na vyuo vya kawaida na nchi hizo zikisaidia kama maeneo ya Mazimbu kipo Chuo Kikuu, Dakawa ipo shule ya wasichana na chuo, Kongwa ipo shule; kwa nini Kilolo tu ndiyo liwekwe gereza? Tunaelewa yapo makubaliano kwa nini hayafanyiwi kazi? Kama sitapata majibu nitashika shilingi ya mshahara wa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, wadau wanaosaidia Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa ni pamoja na Kampuni ya ASAS imesaidizi sana ujenzi wa vituo vya polisi na dawati la mkoa na kadhalika. Pia Kampuni ya Majembe Auction Mart imekarabati gari la polisi Kilolo ambalo litapelekwa kituo cha Ilula. Aidha Silver Land wamesaidia gari la kituo cha polisi Ifunda.

Mheshimiwa Spika, Dkt. Ritta Kabati amefanya ujenzi wa Kituo cha Polisi cha Semtema katika Kata ya Kihesa na kadhalika. Je, Serikali inautambua? Inahamasishaje wadau wengine waendelee kusaidia jeshi hili?

Mheshimiwa Spika, kuhusu stika za Wiki ya Nenda kwa Usalama; je, Serikali inatambua stika zinazouzwa katika Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani zinauzwa na wala mtu halipi kwa control number wala risiti?

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hii mada ya maji kwa sababu maji ni uhai, maji ni ibada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Juma Aweso. Kwa kweli ana haki ya kupongezwa ana haki ya kufanyiwa kila kitu kwa sababu, Aweso amekuwa ni msikivu hata katika Kamati yetu ya Maji, Mheshimiwa Aweso tukienda kumuona sisi Wabunge wenzie amekuwa na msaada mkubwa, kwa hiyo tuna haki ya kukusifia. Pia tumsifie Naibu Waziri amekuwa ni mama ambaye anafanyakazi vizuri sana, anatuwakilisha vizuri sana katika miradi ya maji ni Engineer ambaye kwa kweli anajituma sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe hongera nyingi sana Katibu wetu Mkuu Kaka yetu Sanga ambae amekuwa akifanyakazi kubwa, Naibu Katibu Mkuu ambaye pia ni mama amekuwa akifanyakazi nzuri sana katika Wizara ya Maji. Niwapongeze wafanyakazi wote wa maji wanasema wao ni ndugu na ndio maana wanaelewana wanafanyakazi vizuri hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema kwamba Mheshimiwa Aweso anafanyakazi vizuri, leo ametuletea mawifi wawili kwa kweli tena jasiri hasa na tumeamini kwamba umetulia, umetulizwa na unafanyakazi vizuri kwa sababu wale wakina mama ni jasiri sana na tumewaona kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe pongezi zangu nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia. Mama Samia amefanyakazi nzuri sana kuhakikisha kwamba fedha nyingi zinaelekezwa kwenye miradi ya maji, fedha za UVIKO zinaelekezwa pia kwenye miradi ya maji na sasa hivi tunaamini kabisa tunakwenda kumtua mwanamke ndoo kichwani. Kumtua ndoo mwanamke kichwani tunataka maji yafike mpaka pale alipo nyumbani kwake siyo tunayafuata kilomita 10 au tuyafuate kwenye Kata hapana, tunaomba Mheshimiwa Aweso uangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi nyingi sana kwa Mkurugenzi wa RUWASA na yeye maji vijijini kwa kweli inafanyakazi yake vizuri sana, hongera sana. Lakini naomba pia nimpongeze Mkurugenzi wetu wa IRUWASA Iringa na yeye amekuwa akitusaidia sana katika miradi yetu ya Iringa, anafanyakazi nzuri sana. Lakini siwezi kumsahau Meneja wa RUWASA ambaye ni Engineer Joyce Bahati huyu ni mama jasiri na yeye amekuwa na ushirikiano mzuri, pamoja na Meneja wake wa Wilaya zote za Mkoa wa Iringa, wamekuwa na ushirikiano mkubwa sana kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe katika Kamati ya Maji kwa kweli tumefanya ziara yetu katika Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani, tumeenda kuona miradi mizuri, miradi mikubwa sana, naomba nitoe pongezi kubwa sana kwa Mkurugenzi wa DAWASA ambaye miradi ile mingine ilikuwa imeshindikana muda mrefu, lakini sasa hivi miradi inafanyakazi vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa Diwani Dar es Salaam kulikuwa kuna changamoto kubwa sana ya maji katika Mkoa wa Dar es Salaam, lakini sasa hivi maji yanapatikana ila changamoto yake sasa ni usambazaji wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa pia ulikuwa na miradi sita, miradi ambayo ilikuwa kila siku ukienda kwenye ziara akina mama wanalalamika maji hakuna, ile miradi ni chechefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya Izazi, Mnadani, Fyome, Magunga Wilaya ya Iringa DC, pia kulikuwa na miradi ya Sawala, Mtwango, Ikiziminzowo na Ukami katika Wilaya ya Mufindi, miradi hiyo tuna imani sasa hivi imeanza kufanyiwa kazi na tuna imani sasa akina mama tunaenda kuwatua ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo miradi ambayo tayari inatoa maji natoa pongezi, leo hii niseme miradi ambayo inatoa maji kumpongeza Meneja wa RUWASA pamoja na IRUWASA, ambao wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana pamoja na Mama Samia ambaye ametuletea fedha nyingi katika Mkoa wetu wa Iringa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi kama Ruaha Mbuyuni, Msosa, Mgowelo, Kitelewasi na Lundamatwe, Image, Mawambala na Vitono hii miradi iko katika Wilaya ya Kilolo. Lakini kuna mradi wa Ikweha, Ihigo, Lulanda, Kusonga, Idumika, Uhambi, Lingetu, Nyololo katika Wilaya ya Mufindi, pia tuna miradi kama Mafuruto, Ndiwili, Kilamambo, Mkumbwanyi katika Wilaya ya Iringa DC. Tuna kila haki kwa kweli ya kuwashukuru sana wenzetu wa RUWASA na IRUWASA katika Mkoa wetu wa Iringa hasa Engineer Joyce siku zote umekuwa na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa kuna changamoto ambazo tumekuwa tukizikuta katika miradi hii ya maji, kwanza kabisa TRA kutokutoa vibali vya msamaha vya kodi kwa hiyo inasababisha hii miradi mingi sana kucheleweshwa. Sasa naomba Serikali iangalie hawa TRA vibali vipatikane kwa wakati hii miradi iweze kukamilika kwa wakati, lakini tulivyokwenda pale Dar es Salaam tulikuta wafanyakazi wengi sana ni vibarua au wanafanyakazi kwa mikataba walioajiriwa ni wachache sana. Mimi naomba Serikali waamini hizi mamlaka waweze kuajiri, kuna ngazi ndogo sana kwa nini wasiwaajiri wenyewe? Kwa sababu kwanza kabisa kuna miradi mingine inatekelezwa kwa fedha yao wenyewe ambayo wameikusanya. Sasa kuwaajiri wafanyakazi hawa wachache ni vizuri sana kuliko kusubiri kibali kutoka kwenye Wizara ya Utumishi inasababisha changamoto nyingi sana hata kukusanya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri, kwamba maji yanapatikana kwa mfano hata huko kwetu Iringa kuna mito kuna kila kitu lakini tuna miradi mikubwa katika kila maeneo, tatizo ni fedha ya usambazaji wa yale maji, unakuta wanawake bado wanahangaika wakati tunasoma hapa tumepewa miradi mikubwa ya maji lakini fedha ya kusambazia maji inacheleweshwa sana. Kwa hiyo, niombe Wizara ihakikishe kwamba sasa hivi inatenga fedha nyingi kwa ile miradi ambayo imekamilika ili maji yaweze kusambazwa katika vijiji vyote ambavyo vinatakiwa kupatiwa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna changamoto ya mradi unaweza Kijiji kingine kikarukwa halafu sehemu ile kuna ufugaji kwa hiyo unakuta miundombinu inatobolewa watu wanatoboa lile bomba ili either mifugo wapate maji au wao wapate maji. Kwa hiyo, naomba pia wakati wanasambaza haya maji wahakikishe kwamba kila Kijiji kinapatiwa maji ili kusiwepo na uharibifu wa miundombinu ambayo inasambaza hayo maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba kuwepo na program ya uvunaji wa maji kwa sababu, tunaona kwamba tumekuwa na maji mengi ya mvua ambayo yamekuwa yakiharibu barabara, tukiwa na program ya kuvuna maji hasa katika mashule, katika vituo vya afya, katika nyumba zetu itasaidia hata watoto wetu watakuwa na mazingira mazuri, watakuwa wanatengeneza maua kwa sababu maji yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naomba niunge mkono hoja nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, naomba nami nitoe pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu ambae amefanya kazi nzuri katika nchi hii, amekuwa Rais wa mfano, amekuwa suluhu ya matatizo katika nchi yetu, Watanzania kwa kweli kazi yetu ni kumuombea tu dua Mwenyezi Mungu aendelee kumuweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mkuu wangu wa Mkoa Mheshimiwa Halima Dendegu Mkuu wa Mkoa wa Iringa anafanya kazi nzuri sana katika Mkoa wetu tunampenda sana. Pia naomba nimpongeze Waziri Mwenye dhamana Angela Kairuki, Rais hakufanya kosa kumchagua nafasi aliyokupa chapa kazi nasi tuko nyuma yako Mwenyezi Mungu atakujalia, pia Naibu Mawaziri ambao yuko nao tunajua pia ni wachapakazi wazuri sana, endeleeni kuisaidia TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze TARURA kwa kazi nzuri sana, naomba kwa kweli waongezewe bajeti kwa sababu kwa kipindi kifupi tu wameonesha kazi nzuri anayoifanya. Niunge Mkono wale waliosema Seif apewe tuzo, chifu wetu apewe tuzo naunga mkono na apewe kweli kwa sababu kwa kazi nzuri ambayo barabara nyingi sana za vijijini zimefunguka na hata vifo vya akina Mama na Watoto vimepungua, Mungu ambariki sana. Pia nimpongeze TARURA Mkoa wetu wa Iringa yuko vizuri anafanya kazi vizuri, Mwenyezi Mungu ambariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kumpongeza Rais wetu kwa pesa za UVIKO na pesa za tozo ambazo alizitoa katika Mkoa wetu wa Iringa zimeongeza bajeti, karibu asilimia 200 ya bajeti kutoka Bilioni 6.3 hadi Bilioni 16.7. Ongezeko hilo limefanya barabara nyingi kuweza kujengeka za lami hata za changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, bado zipo changamoto katika Mkoa wetu kutoka na jiografia yetu ina milima mimgi ambayo barabara zake nyingi zinahitaji madaraja mengi na wakati wa mvua huu barabara nyingi sana hazipitiki wakati wa masika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya barabara ambazo zina changamoto kubwa sana naomba tu nizitaje kwa uchache. Katika Wilaya ya Iringa kuna barabara ile ya Izazi – Mboliboli kilomita 25, kuna Mtwivira – Ikongo kilomita 1.5, Mufindi kuna barabara ile ya Tambalang’ombe – Kwa Mtenga kilomita 41, Luganga – Itimbo – Isupilo kilomita 11. Wilaya ya Kilolo kuna barabara ya Muhanga – Mugeta kilomita 18, Ilula – Uhambingeto – Ulambilelo kilomita 17, Mtandika – Nyanzo kilomita 40, Itimbo – Kitelewasi kilomita 26, Ilula – Ibumu kilomita 20. Pia kuna barabara kutoka Kitowo kwenda mpaka Masisiwe hii barabara mpaka sasa hivi nilipita juzi tu ina changamoto nyingi sana. Kwa hiyo, ninaomba TARURA iziangalie hizi barabara hizi barabara ili Mkoa wetu wa Iringa uweze kufunguka kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao upungufu mkubwa sana wa watumishi wa kada zote katika Mkoa wetu wa Iringa. Nikichukulia tu kada ya afya watumishi wanaotakiwa ni 4,647 na waliopo 2,416 upungufu kama 2,111 kama asilimia 48. Tunaomba Wizara sasa katika hizi ajira mpya iangalie kwa jicho la kipekee Mkoa wetu wa Iringa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tupongeze ujenzi na ukarabati wa shule zote nchini lakini sasa waangalie pia Walimu wetu waboreshewe nyumba zao zijengwe na hasa huko Vijijini na zikarabatiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Madiwani wenzetu pia wanachangamoto nyingi sana, Mimi ni mjumbe wa ALAT. Zipo changamoto ambazo tuliainisha tulitegemea sana zingefanyiwa kazi, wanafanya kazi kubwa kwa kweli changamoto ni nyingi waangaliwe na waboreshewe maslahi yao ili waweze kufanya kazi vizuri kwa sababu miradi yote ipo chini yao. Hata Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Mitaa pia waboreshewe posho zao kwa sababu wanasimamia miradi pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitambue wadau wa maendeleo wanaochangia katika Mikoa yetu lakini wanasaidia pia katika bajeti yetu. Katika Mkoa wetu yuko mdau Mkubwa MNEC wetu mpendwa Ndugu Salim Asas, ameweza kutoa kwanza Shilngi Milioni 100 kwenye majengo ya Machinga, amechangia ujenzi wa jengo la Ustawi wa Jamii ambalo ni la mfano na Waziri Mkuu alilifungua. Pia amejenga jengo la damu salama, amejenga jengo Watoto Wachanga, ujenzi wa ICU, jengo la viungo bandia, jengo la wagonjwa maalum (VIP) lakini huwa anatoa maziwa kwenye shule zote. Mdau huyu ni wa kuigwa nchi nzima na siku nyingine aletwe hapo tumpigie makofi ili wengine waweze kumuiga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo ya Wazabuni, wanapata shida sana, naomba kabisa Wazabuni hawa wamekopa benki, wanalipa riba, TRA wanatozwa zile penalty, usumbufu mkubwa sana wanakwenda huko hazina, naomba waangaliwe kwa kweli na tuambiwe kwamba wazabuni wako wangapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu asilimia 10. Kuna watu hawakopesheki, kuna wamama ambao wamezaa watoto wenye ulemavu, hawa watu hatujajua wamewekwa kwenye kundi gani? Wanabeba watoto kuanzia asubuhi mpaka jioni, wanatafuta pesa kwa ajili ya kuwasaidia hawa Watoto, bado Serikali haijajua kwamba je, hawa watu wanakopa kule kwa watu wenye ulemavu au kwa hawa wamama wa kawida? Kwa sababu, hebu tuangalie mimi nakuomba Mheshimiwa Angela Kairuki wewe ni Mama mwenzetu naomba utakapokuja utujibu hawa wamama wapi wakope? Wako kwenye kundi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hautatoa jibu nitashika shilingi nitaomba Wabunge wote watuunge mkono ili hawa wamama wajue wanakopesheka katika fungu gani, kwa sababu wote humu ndani ni walemavu watarjiwa, lakini hawa wanawake wengine wamewakimbia na waume kwa sababu wamezaa watoto wenye ulemavu. Jamani hili jambo ninalisema kwa uchungu mkubwa ninaomba Bunge hili kwa kweli hebu liangalie na tutoke na suluhu. Tumeuliza sana maswali lakini hatupatiwi majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana na Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi lakini vile vile nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata hii nafasi ya kuchangia saa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa leo ni siku ya Mwanamke wa Bunge naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Spika wetu wa Bunge ambaye ni mwanamke namba moja kwa kazi nzuri sana ambazo amekuwa akizifanya hapa Bungeni, lakini vile vile hata katika Jimbo lake hata kwa tuzo nyingi ambazo amekuwa akizipata kwa kweli anastahili. Tunampongeza sana sana sisi wanawake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pongezi zangu nyingi sana kwa Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko kwa kweli Wizara hii ya ameitendea haki. Ameitendea haki kwa sababu amekumbuka hata wanawake wachimba madini. Tunamshukuru pia tumeweza kutembelea wanawake wengi sana wachimba madini, wengi wanamshukuru. Kuna fursa nyingi sana sasa hivi wana hamu hata ya kuchimba madini kwa ajili yake. Mwenyezi Mungu ambariki sana Doto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumpongeze Naibu Waziri Dkt. Kiruswa na yeye amekuwa msaada sana katika hii Wizara na kuhakikisha kwamba inakwenda vizuri. Nimpongeze pia Katibu Mkuu wa Wizara kaka yetu Heri anafanya kazi nzuri sana pamoja na watendaji wote wa Wizara hii ya Madini niombe wachukue, niwapongeze pia Kamati ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kupongeza Wizara hii kwanza kwa kuweza kuongeza pato la Taifa kutoka walikuwa wana 7.8% mwaka 1921 na sasa hivi wamefikisha point tisa point saba mwaka 2022. Mheshimiwa Rais wetu aliwawekea lengo kwamba wafikishe angalau 10% na unaona sasa hivi wana 0.3% tu na ninaimani kabisa kutokana na kazi yao nzuri watavuka lengo kwa hiyo, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa pia na sisi tuna Mgodi unaitwa Nyakavangala. Huu Mgodi uko katika Jimbo la Isimani nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri ulikuja Nyakavangala tulipouliza maswali hapa Bungeni na ukakutana na wawekezaji wa Nyakavangala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakushukuru kwamba ulikuja kuona kulikuwa kuna changamoto nyingi sana na bado zipo vilevile. Ulikuwa umeagiza GST wawasaidie ule mgodi lakini toka ulivyotoka bado hawajaenda kufanya kitu chochote. Kwa hiyo, tunakuomba endelea kuwahimiza waende ili hawa GST wakasaidie huu mgodi na sisi tuweze kupata wawekezaji pia lakini waweze kupatiwa fedha ili nasisi tuwe kama, tupate wawekezaji kama GGM ili na sisi Wanairinga tuweze kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa wapo wachimbaji wadogo wadogo. Kwa mfano Mwenyekiti kule kwake kule Mufindi wananchi wanachimba wadogo wadogo lakini hawajapimiwa wanachimba tu bila kujua kwamba wanatakiwa wafanyaje. Kwa hiyo, tunaomba sasa Wizara hii GST waje wapime katika Mkoa wetu wote wa Iringa ili wachimbaji wadogo wajue maeneo halisi ya uchimbaji ili kinamama, vijana, na Wanayalukolo wote wa Iringa waweze pia kujiajiri kupitia madini na pia tuongeze pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana STAMICO, nimpongeze Mtendaji Mkuu wa STAMICO na Bodi nzima kwa sababu STAMICO zamani tulikuwa tunajua ni shirika ambalo linaweza likafa wakati wowote lakini sasa hivi huu uongozi umefanya tunaona STAMICO sasa inafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona wameweza kubuni miradi ya kupunguza hata uharibifu wa mazingira kwenye migodi nchini lakini pia kuna mradi ule wa kuongeza kipato mkaa wa mawe wameendelea kuingia ubia kazi ya uchorongaji pamoja na GGM na tulishuhudia siku ile tulivyokuja Geita wameingia Mkataba wa karibu shilingi bilioni 52.2 kwa hiyo, ni kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia STAMICO wamekuwa mara nyingi sana wakiwasaidia watu wenye ulemavu vifaa vya uchimbaji. Tunawapongeza sana. Tunaomba pia hata wako, hawa tunaona watu wenye ulemavu wanaume lakini wako pia watoto wa kike pia wako wana kikundi chao, tunaomba pia muwasaidieni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mara nyingi wamekuwa wakiwasaidia pia hata wanawake wachimbaji. Tunaomba muendelee sasa kulea wanawake wachimbaji nchini kwa sababu wameonyesha mwamko mkubwa sana na muweke kabisa jicho la kipekee ili kuwapatia sasa utaalam maana yake ndiyo vitu ambavyo wanavikosa; utaalam na vifaa vya uchimbaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunashukuru hata Mheshimiwa Waziri alikiri kuwa wanawake wengi ambao wameingia kwenye mambo ya uchimbaji wamekuwa wakilipa vizuri kodi na mapato na kwa uaminifu sana kwa hiyo tunazidi kuwapongeza wanawake wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuwapongeza wanawake wote wachimba madini nchini. Kupitia Chama chao cha TAOMA tumeweza kubaini changamoto nyingi sana baada ya kukutana na chama hiki cha wachimba madini nchini pamoja na wanawake wanaochimba madini. Kwanza kabisa hawana mitaji ya kutosha katika kuweza kuchimba haya madini lakini vilevile tunaona kwamba vifaa, hawana vifaa kabisa vya kuchimbia na uchenjuaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baya zaidi hawakopesheki kabisa kwa sababu hawana dhamana za kuweka. Kwa hiyo sasa naomba sasa mabenki wawakopeshe basi hawa wanawake wachimba madini. Tunawaomba STAMICO kwa sababu wao ni walezi basi watoe dhamana wawadhamini hawa wanawake waweze kukopesheka ili wachime kwa urahisi na waweze kufanya kazi yao vizuri kwa sababu kina mama wengi zamani walikuwa wanakuwa tu mama lishe, hawafanyi kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba tumpongeze Mwanamke mwenzetu ambaye yeye amekuwa mwekezaji wa Mgodi wa GGR pale Geita. Kwa kweli na amekubali pia kuwa mlezi wa wachimbaji wanawake wadogo wadogo nchini Dada yetu Sarah Masasi, tunampongeza sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaomba sasa Wizara iweke mkakati wa kuwasaidia Watanzania waliowekeza katika hizi refinery ili wapate malighafi kwa sababu changamoto pia wamewekeza, wameweka fedha zao nyingi wamekopa benki lakini unakuta malighafi za kwenda kwenye hizi refineries hakuna. Kwa hiyo, kuwepo na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba malighafi inakwenda pale ili wathaminishe hizi dhahabu kabla hazijapelekwa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nikushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niwashukuru na Wabunge wenzangu wote na pia nishukuru wanawake wote kwa sababu leo ni siku yetu basi tunawashukuru pia Uongozi wa Bunge kwa kuona umuhimu na sisi wanawake tuwe na usiku wetu na Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Wanasema moyo usiokuwa na shukrani hukausha mema yote, kwa niaba ya familia ya Mwamoto naomba nitoe shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Spika na Wabunge wote wa Bunge hili la Muungano kwa kutufariji wakati wa msiba. Kwa kweli hatuna cha kuwapa lakini Mwenyezi Mungu awabarika sana na marehemu alikuwa ni Mume wa Askari wa Gereza Kuu la Iringa. Pia, naomba nishukuru sana Mheshimiwa Waziri ulipiga simu na ukatuletea na mchango Mungu akubariki sana lakini naomba pia niwashukuru RPC pamoja na Uongozi mzima wa Magereza Mkoa wa Iringa kwa ushirikiano wao mkubwa ambao waliuonesha wakati wa msiba wa Kaka yetu mpenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais ambaye ndiye Amiri Jeshi Mkuu kwa maboresho makubwa sana katika Jeshi hili, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa ushirikiano wao mkubwa katika Wizara hii, wamekuwa watu wa msaada sana wakati wako tayari. Naomba pia niwapongeze Wakuu wote wa Majeshi ambao wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana bila kumsahau Anna Makakala ambaye anatuwakilisha wanawake vizuri katika jeshi hilo. Naomba pia nimpongeze RPC wetu wa Mkoa wa Iringa amekuwa na ushirikiano mzuri sana katika Mkoa wetu wa Iringa na kazi nyingi zinakwenda kwa sababu yuko tayari wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Polisi pale Kihesa tumekuwa tukiongea muda mrefu sana, wameanza angalau kujenga, japokuwa nyumba zile hazitoshi, bado maboresho yanahitajika sana katika nyumba zile za FFU Kihesa. Pia nyumba zilizopo Makao Makuu pale Iringa, kambi zao kwa kweli ni mbovu sana. Wakinamama, watoto ambao wanakaa katika zile kambi wanaishi kwa shida sana, tunaomba kwa kweli pia ziboreshwe ili waweze kuishi vizuri kwa sababu Askari wengi wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie kuhusu Wilaya ya Kilolo. Wilaya ya Kilolo imeanza siku nyingi sana toka 2022 lakini haijajengewa Makao Makuu ya Polisi katika Wilaya ya Kilolo. Sasa utakuta OCD anakaa Kata ya Lugalo karibu kilometa 70 kutoka yalipo Makao Makuu lakini Serikali inatumia gharama kubwa sana kusafirisha mahabusu kutoka huko Lugalo mpaka katika Mahakama ambayo ni Makao Makuu. Kwa hiyo, ungefanyika utaratibu mzuri kwamba Makao Makuu kwanza ijengwe ili OCD akae na DC sehemu moja, kupunguza hata gharama za Serikali lakini pia hata mahabusu wasiwe wanasafirishwa kwa muda mrefu kwa sababu hata kuna uhaba mkubwa sana wa magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ni kulipia tu lile eneo kwa sababu eneo lipo lakini halijalipiwa, tulisikia Serikali ilishaanza kutenga pesa kwa ajili ya ujenzi wa Makao Makuu ya Polisi Kilolo lakini eneo halijalipiwa, kwa hiyo, ufanyike utaratibu lile eneo walipe fidia kwa wananchi ili waweze kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kituo cha Polisi cha Ruaha Mbuyuni kipo mbali sana na Makao Makuu hakina gari lakini kumekuwa na ajali nyingi sana katika ile Barabara, sasa tunaomba Serikali iangalie umuhimu wa kutoa gari katika Kituo cha Polisi cha Ruaha kwa sababu kiko karibu kabisa na Jimbo la Mikumi. Pia, tunaomba Serikali itoe pesa kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi Idodi ambacho ni lango kuu la utalii kwa ajili ya kusaidia Mikumi National Park.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalipongeza pia Jeshi la Magereza linafanya kazi nzuri sana, kuna mashamba makubwa ambayo kwa kweli kama yatafanyiwa kazi nzuri nafikiri Jeshi la Magereza litakuwa na uchumi wa kutosha. Kuna lile Gereza la Isupilo, kuna Gereza la Pawaga, wana mashamba makubwa ambayo yamekaa hayana kitu chochote, sasa kama hawawezi basi waweke hata wawekezaji waweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ritta muda wetu ndio umeisha, unga mkono hoja.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia jioni hii ya leo. Naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu. Naomba nianze na pongezi kubwa, niungane na wachangiaji wote waliompongeza Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutangaza utalii kwa kupitia Royal Tour. Pia niungane na wote ambao wamekuwa wakikuombea wewe kugombea Urais katika Mabunge na nina imani kabisa kwamba hiyo nafasi utakayoigombea tunakuja kuweka historia katika Bunge letu hili la Jamhuri ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri wetu Mheshimiwa Mchengerwa ambaye kwa kweli kwa kipindi tu kifupi ameweza kuonesha kwamba Wizara hii inaanza kubadilika na inaleta maendeleo mazuri. Pia nimpongeze Naibu Waziri, wifi yangu ambaye pia amefanya kazi nzuri sana katika Wizara hii, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie kuhusu Mradi wa REGROW; kusema kweli kabisa Mradi REGROW kama walivyosema wenzetu wote waliochangia asubuhi na sasa hivi, ni mradi ambao tulikuwa tunategemea sasa utakuza utalii katika Mikoa yote ya Kusini lakini tunaona bado mradi huu unasuasua. Toka ulipoanza mwaka 2019 sasa hivi tuna miaka mitano, lakini bado tunaona hakuna chochote kinachowekezwa katika Mkoa wa Iringa, maana yake tuliambiwa kungejengwa kituo kikubwa cha maonesho ya utalii wa kimataifa katika Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Spika, pia walisema wangejenga ofisi ya kanda, lakini tunaona mpaka leo hii bado. Je, ni lini sasa vitu hivi vitajengwa, lakini pia nataka kujua je, wananchi wameandaliwa kiasi gani kuupokea huu mradi, kwa sababu tunategemea huu mradi sasa watajiajiri kwa kutumia utalii kama ilivyo kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kutuletea pesa kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa ndege. Tunategemea huu uwanja wa ndege pia utahamasisha sana utalii katika Mkoa wetu wa Iringa na Nyanda za Juu Kusini, lakini sasa tulikuwa tunaomba pamoja na huu ujenzi bado wanatakiwa wajenge ile barabara inayokwenda katika mbuga za Wanyama, Ruaha National Park kwa sababu kukiwepo tu na huu uwanja bila kujengwa ile barabara bado tutakuwa hatujafanya chochote.

Mheshimiwa Spika, tunategemea hata utalii wa ndani utaongezeka, lakini vilevile tunaomba pia katika lile lango pale Idodi kijengwe kituo kikubwa cha polisi kwa ajili ya usalama wa watalii kwa sababu tumeona kuna kontena tu ambapo sio vizuri. Pia wangesaidia hata ujangili ambao unatokea pale, kituo kile kitasaidia, wapewe na gari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Iringa lipo eneo ambalo tunaomba Serikali ibadilishe matumizi ili gereza lile liondolewe eneo hilo litumike kama kivutio cha utalii. Eneo la Kihesa Mgagawa ambalo lipo katika Wilaya ya Kilolo, Mkoani kwetu Iringa. Hili eneo lilitumika na wapigania uhuru wa Kusini mwa Afrika, walilala pale akina Mandela, walikuwepo akina Sam Nujoma, walikuwepo Walter Sisulu, Thabo Mbeki. Hawa watu ni maarufu sana sasa kuweka gereza sidhani kama tunawatendea haki, na hiki ni kivutio ambacho kingeweza kuwavuta watu wote katika nchi zao waje waone wapigania uhuru walikuwa katika maeneo gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka Balozi aliishawahi kuja kutembelea lile eneo alisikitika sana kukuta kwamba kuna gereza. Nashauri ni bora hata kijengwe chuo cha utalii lakini pia hayo maeneo yatumike kwa utalii ili tuweze kutengeneza pesa. Pia itasaidia hata wananchi ambao wapo Kihesa Mgagao kujiajiri kwa kutumia utalii na barabara nyingi za pale zingetengenezwa. Hao watu ambao marais wao walikuwa wamekaa katika kile kituo wangekuwa wanakuja kutalii na ingesaidia kuongeza pato la utalii katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niungane na wale wote waliozungumzia kuhusiana na tatizo la ndovu. Katika Mkoa wetu wa Iringa ndovu pia wamekuwa wakileta uharibifu mkubwa. Yapo maeneo ambayo yameathirika na tembo na haya maeneo mengi ni yale ambayo yamezungukwa na Ruaha National Park. Katika Jimbo la Isimani kuna Kata ya Idodi, Mlowa, Pawaga, Unyinga na kadhalika. Pia katika Jimbo letu la Kilolo kuna Mahenge, Nyanzwa na Ruaha Mbuyuni na changamoto kubwa kabisa ya hawa watu ni fidia ambayo wanapewa fidia kidogo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa ahsante sana. Malizia sentensi kengele imeshagonga.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba, pengine sasa hawa watu ambao wapo katika haya maeneo waweze kupatiwa hata miradi midogo midogo kama ufugaji wa nyuki ili waweze kusaidia. Tumesikia kwamba nyuki huwa wanasaidia kufukuza tembo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nichangie katika Sekta hii ya Kilimo ambayo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtangulize Mwenyezi Mungu katika mchango wangu. Naomba nitoe pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Waziri Bashe kwa Naibu Waziri Anthony Mavunde, Katibu Mkuu Andrew Massawe na watendaji wote wa Wizara kwa kuhakikisha kwamba kilimo kinaweza kubadilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona sasa mapinduzi ya kilimo kweli kweli, wananchi wanategemea sana, wanamwamini sana Mheshimiwa Bashe kwa mambo makubwa ambayo ameyafanya. Naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Suluhu kwa hotuba yake ya siku ya tarehe 24, siku ambayo walikuwa wanagawa vifaa vya wagani wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu siku ile Maafisa Ugani wamepewa vifaa, lakini naomba wapatiwe elimu, hiyo elimu iendane na maeneo ambayo tunatokea. Kwa mfano, Mkoa wetu wa Iringa tunalima mahindi, chai, pareto, alizeti, parachichi basi wale Maafisa Ugani wawe angalau wana elimu ya hayo mazao ambayo tunayalima katika maeneo yetu ili rahisi kwa sababu Wizara imeanzisha mashamba darasa inakuwa rahisi hata kutoa elimu kwa wakulima na kilimo kitakuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua bado tuna upungufu kiasi gani wa Maafisa Ugani ili tuweze kujua kwamba watatusaidiaje. Pia nataka kujua tunao vijana wetu ambao wamehitimu masomo ya kilimo katika vyuo vyetu nchini. Hawa vijana wako katika wilaya zetu, halmashauri zetu lakini je, Serikali haiwezi kuwachukua wakasaidia hata katika haya mashamba darasa? Kwa sababu tulivyokuwa zamani tuna upungufu wa Walimu tuliwachukua Walimu katika masomo ya sayansi wakawa wanajitolea. Huu ndio uzalendo, lakini vijana wetu wamekatwa, wamehitimu masomo yao vizuri, wamekaa hawafanyi kitu chochote. Tunaomba pia hili Serikali iliangalie ili tupunguze hata upungufu wa Maafisa Ugani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipongeze Serikali kwa mambo yafuatayo:-

(a) Kuongeza pesa ya utafiti;

(b) Kuongeza eneo la umwagiliaji;

(c) Upatikanaji wa mbegu bora;

(d) Ununuzi wa nafaka; na

(e) Ushirika na masoko ya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbolea tunaomba Mheshimiwa Waziri ajitahidi. Mbolea ukienda kila sehemu, kila mkutano, changamoto kubwa ni bei ya mbolea. Kwa hiyo tuna imani kabisa kwamba sasa hivi tumesema kwamba kuna kiwanda, lakini ulikuwa unaomba ruzuku kwa ajili ya mbolea ili bei iweze kupungua kabisa, maana yake wakulima wengi wameshindwa hata kulima sasa hivi, wamevuna eneo dogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lingine, naomba pesa ya utafiti ipelekwe kwa wakati ili hizi tafiti ziweze kufika kwa wakulima, kwa sababu changamoto kubwa ya utafiti kwamba tafiti nyingi zinafanyika, lakini hazifiki kwa wakulima. Kwa hiyo kilimo kinakuwa hakina tija kwa sababu zile tafiti zinafanyika, lakini zinakaa katika vituo vya tafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze uwekezaji wa eneo la umwagiliaji. Kwa kweli na niwapongeze sana kwa sababu hata katika Mkoa wetu wa Iringa tuna miradi mingi ya umwagiliaji, lakini wametukumbuka katika Mradi wa Mgambirenga katika Wilaya ya Kilolo. Kwa hiyo niombe, kwa sababu umwagiliaji ndio kilimo kinachotakiwa, ndio kilimo cha uhakika. Umwagiliaji kwa mfano, Zimbabwe mabenki hayawezi kukukopesha kama hulimi kilimo cha umwagiliaji. Kwa hiyo niombe na sisi sasa tuweke pesa nyingi katika umwagiliaji ili wakulima wengi wamwagilie ili tuwe na uhakika wa mazao yetu tunayoyalima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunashukuru sana katika Mkoa wetu wa Iringa wameweza kutupatia fedha kufufua zao la chai katika Wilaya ya Kilolo. Wilaya ya Kilolo watu walikuwa wamekata tamaa kabisa kwamba sasa hivi hatuwezi kabisa, tunaichukia na Serikali. Mheshimiwa Naibu Waziri alikwenda Kilolo akawaahidi na sasa hivi hii Serikali ni Sikivu, inatoa pesa na zao sasa la chai katika Wilaya ya Kilolo linafufuka, Halmashauri ya Kilolo itapata pato, wananchi watapata pato na Serikali itaongeza pato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kuhusu kilimo cha mbogamboga. Kwa kweli sekta hii ni ndogo lakini inaongoza katika mapato ya export na mapato ya soko la ndani. Hapa naomba nimpongeze Dkt. Jacqueline Mkurugunzi wa TAA pale Arusha. Kwa kweli tulimtembelea pale Arusha, amesaidia sana katika kuhakikisha kwamba mbogamboga na matunda Tanzania sasa hivi inawezekana. Nipongeze pia hata Serikali yetu kwa kutafuta soko la parachichi. Lakini nimpongeze pia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia pongezi yako.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Hadija Jabiri pale Iringa na yeye anatusaidia sana katika zao la mbogamboga na matunda ambako wanawake wengi sasa hivi tumejikita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nitaandika kwa maandishi kwa sababu naona kwamba point zangu zingine sijazitoa, lakini namshukuru Mungu…

MWENYEKITI: Pole sana Mheshimiwa Ritta Kabati.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hii Procurement Act.
Kwanza kabisa na mimi nianze kumpongeza Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kuleta hii sheria kwa sababu tumekuwa tukiipigania muda mrefu sana na tunaamini sasa uletwaji wa hii sheria itatusaidia pia hata Serikali kuongeza pato la Serikali na watu ambao walikuwa wanakwepa kulipa kodi na wale ambao walikuwa wanafanya tender kwa upendeleo hasa angalau itasaidia hii sheria kuleta haki sawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze Kamati ya Bajeti kwa sababu kwa kipindi tu kifupi wameweza kutuletea hotuba yao nzuri japokuwa tumechelewa kuisoma, lakini ninaimani kwamba sheria hii sasa inaenda kutendewa haki. Pia nimpongeze Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa sababu siku zote huwa anakuwa anatuletea sheria nyingi, lakini tunakuwa hatumpongezi, nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kupongeza Serikali kwa kuiondoa GPSA kupanga bei kwa sababu kwa kweli ilikuwa ni tatizo kubwa sana kwa kutupangia bei kwa wazabuni.
Mheshimiwa NAibu Spika, jambo la pili, nilikuwa nataka kujua hii GPSA bado ilikuwa inachagua wazabuni wachache ili waweze ku-tender hizo zabuni. Sasa je, katika sheria hii inasemaje maana yake zamani wakati GPSA haipo hizi tender zilikuwa zinatangazwa magazetini na kila mtu anatendewa haki, ku- tender hizo zabuni. Sasa labda sheria ituambie je, GPSA wameondolewa na ile kuchagua wazabuni wachache katika ku- tender hizi zabuni?
La pili pia hii GPSA ilikuwa inatoza ile asilimia mbili ya gharama ya mkataba je, na hii asilimia mbili imeondolewa? Nilikuwa nataka nipatiwe majibu ya hilo pia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, ukisoma hotuba ya Waziri ukurasa wa saba namba “E”, niipongeze kwa sababu imeweka mfumo utakaotoa upendeleo kwa makundi maalum kwa akinamama, vijana, wazee na makundi maalum ya walemavu. Lakini nilikuwa naomba labda sheria hii ingeweka wazi, je, ni asilimila ngapi sasa hayo makundi yatapatiwa? Labda nitoe mfano, kama watatoa asilimia 30, kwa sababu kina mama wengi sana wamekuwa wakifanya biashara tunaona kabisa tofauti labda na vijana na haya makundi mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, labda kama itatoa asilimia 30, ingetamka kwamba asilimia 15 basi wapatiwe akina mama na asilimia 15 yagawane haya makundi mengine. Hili litawasaidia akina mama wengi sasa hivi wamekuwa wakifanya biashara lakini wanaona kwamba hawapatiwi huo upendeleo ambao watapatiwa sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukisoma pia kipengele “G” namba hiyo saba inasema kwamba; kuweka sharti la kutumia mfumo wa electronic katika ununuzi na kuongeza uwazi na uwajibikaji. Labda kanuni zingeeleza jinsi ya kuelimisha kutumia hizi mashine za EFDs kwa sababu itasaidia kama wangewekewa uwezo wa kujua hizi mashine, kwa sababu utawakuta akina mama wengine wako huko vijijini, hakuna umeme, hakuna nini, sasa labda wangetoa elimu na kuwajengea uwezo ili waweze kuzitumia hizi mashine kuliko ilivyo, haijaeleza vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nilikuwa naomba labda katika sheria hii tungeona kipaumbele cha Serikali kuwalipa wazabuni kwa wakati. Kwa sababu utakuta kwamba zamani wazabuni Serikali ilikuwa haiwalipi kwa wakati, wanaweza wakapewa tender labda kwenye mashirika au taasisi za umma, lakini malipo yao yanachukua muda mrefu sana. Je, hii sheria sasa itaibana Serikali kuweza kuwalipa hawa wazabuni kwa wakati? Kwa sababu utakuta wazabuni wanadaiwa na wazabuni wanatakiwa sasa waki-issue invoice, wanatakiwa pia watoe risiti na TRA wanatakiwa sasa wakusanye kodi kwa hao wazabuni. Lakini wazabuni hawajalipwa, TRA wanawadai, na TRA usipolipa wao wanatakiwa wakupige penalt. Sasa je, sheria hii inamlindaje mzabuni?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango wangu huo, naomba tu kuunga mkono sheria hii.
Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli Tanzania wa Mwaka 2017
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Muswada huu. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali yetu kwa kuleta Muswada huu pamoja na kuwa ulichelewa sana, lakini nashukuru kwamba umeweza kuletwa.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze pia Wanasheria wa Bunge kwa kweli walitusaidia sana kuhakikisha tunavielewa baadhi ya vifungu sisi Wajumbe wa Kamati ya Miundombinu kwa sababu Muswada huu kidogo ulikuwa ni mgumu kwetu na mpaka ulituletea matatizo wewe unajua, lakini tunawashukuru sana Wanasheria na tunamshukuru sana pia Mwanasheria Mkuu ambaye kwa kweli alijitahidi kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba huu Muswada unaingia humu ndani bada aya kuishawishi Kamati.

Mheshimiwa Spika, pia nisisahau kuipongeza Kamati ya Miundombinu na Mwenyekiti kwa sababu najua kwamba huu Muswada tumeutendea haki muda mrefu sana umeletwa kwenye Kamati yetu na tukaweza kuuchambua na kuna ushauri mwingi sana tuliutoa na tuipongeze Serikali kwamba mambo mengi sana ambayo Kamati ya miundombinu ilikuwa imeomba kwamba yabadilishwe kwa kweli walileta na tukayafanyia marekebisho.

Mheshimiwa Spika, naomba tu kuishauri Serikali kwamba, Miswada kama hii ambayo ina manufaa kwa Serikali angalau tuwe tunapatiwa semina za kutosha hasa Bunge zima ili tuweze kuishauri vizuri Serikali kwa sababu hata sisi Kamati tuliomba muda mrefu sana tuwekewe semina ili tuweze kuuchambua vizuri huu Muswada kwa ajili ya manufaa ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1973 Serikali ilianzisha chombo kama hiki kilichokuwa kinaitwa NASACO, lakini itakumbukwa kuwa, kufilisika kwa NASACO kulisababishwa kutokuwepo kwa Taasisi ya Serikali katika uwakala wa meli na hivyo Serikali kutokuingia moja kwa moja katika kuona nyaraka ambazo zilikuwa zinaingizwa katika shehena. Kwa hiyo, utaona kwamba sasa hivi huu Muswada utasaidia Serikali yetu itakuwa inaweza kuona nyaraka ambazo zipo katika meli ambazo zinaingia na kutoka.

Mheshimiwa Spika, tangu mfumo wa biashara huria uruhusiwe katika sekta hii mwaka 1999, udhibiti haujawahi kuwa mzuri licha ya maboresho kadhaa ya Sheria. Baadhi ya Sheria zilifanyiwa marekebisho lakini hazikujitosheleza kama Sheria ya SUMATRA ya mwaka 2002, Sheria ya Uwakala wa Meli ya mwaka 2002 na Sheria ya Udhibiti wa Mizigo ya mwaka 1981. Upungufu wa Sheria hizo ulisababisha changamoto mbalimbali ambazo zilichangia upotevu mkubwa wa mapato na kukosesha nchi yetu manufaa ya kuwa na Bandari.

Mheshimiwa Spika, labda tu nitoe mfano kwa sababu nishawahi kwenda kutembelea huko Singapore utaona kwa
wenzetu Singapore, Bandari yao ndiyo uchumi wao na wanafanya vizuri sana. Sisi tulikwenda kuona kwa sababu ule Muswada na wao wana chombo kama hiki, kwa hiyo utakuta kwamba wana Sheria ambazo wamezitunga hazina mianya ya rushwa rushwa, hazina mianya ya kuachia wafanyakazi wa Serikali kuweza kuingiza vitu ambavyo vilijitokeza katika NASACO. Kwa hiyo, nashauri Serikali yetu na yenyewe pamoja na kwamba tunapitisha huu Muswada lakini iweze kuzingatia, itengeneze Sheria ambazo zitadhibiti ile mianya ambayo ilisababisha hata NASACO kufilisika kwa sababu utakuta kuna wajanja tu wachache waliacha nafasi kidogo ile mianya wakaweza kuua hii NASACO, kwa hiyo naiomba kabisa Serikali iangalie na izingatie.

Mheshimiwa Spika, sipendi kuchangia sana kwa sababu tayari nafikiri Kamati yangu ya Miundombinu imeweza kutoa ushauri mkubwa sana na naomba kabisa Serikali ichukue ule ushauri wa Kamati kwa sababu ndiko na mimi nilikuwa huko ili iweze kupitia ule ushauri ili iweze kuboresha hiki chombo. Tuna imani kabisa huu Muswada utakapopita, basi tutaitendea haki Bandari yetu na kwa kweli hata hizi nyaraka zote za usafirishaji zitadhibitiwa na chombo cha Serikali na vile vile rasilimali zote za madini, petrol zitasimamiwa na chombo hiki cha Serikali.

Mheshimiwa Spika, huu Muswada ni muhimu sana na niwaombe tu Wabunge wote waweze kupitisha na wasiwe na wasiwasi kwa sababu tunajua kwamba tulikuwa na Muswada wa Makinikia ule ambao Wabunge wengi walikuwa wameonesha wasiwasi lakini saa hivi kutokana na jinsi ambavyo Sheria zimekaa vizuri na zikaweza kupitishwa hata huu pia nina imani kabisa kama tutaupitisha na tukauwekea Sheria nzuri nina imani kabisa sasa Bandari yetu tutaitendea haki.

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo, kwa kweli nishukuru na niombe Wabunge wote tupitishe huu Muswada ili nchi yetu iweze kutendewa haki,