Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Faustine Engelbert Ndugulile (17 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika Mpango wa Maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa uwasilishaji mzuri pamoja na heka heka ambazo tumezipata mwanzoni mwa wiki, lakini Wahenga wanasema kawia ufike. Naomba nijielekeze moja kwa moja katika Hotuba na mapendekezo ya Serikali kuhusiana na Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja, pamoja na vipaumbele vyote ambavyo tumeviweka, ningependa kuona Serikali inaweka kipaumbele katika ujenzi wa reli ya kati. Naungana na Wabunge wote wa mikoa yote ambao wamekuwa wanaliongelea suala la reli ya kati. Tukitaka kupaisha uchumi wetu, tukitaka kuimarisha uchumi wetu bila ya kuwa na reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge naamini kabisa tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, Serikali itakapokuja kufanya hitimisho tunataka kauli iliyokuwa thabiti na wala isiyopinda kuhusiana na nini mikakati yetu ya kujenga reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge, tumeliongea sana, tuliliongelea katika Bunge la Kumi, sasa umefika muda wa utekelezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tungependa kusikia na kuona Mpango wa Serikali katika kuimarisha Bandari ya Dar es Saalam, tuipanue, kuna kazi kubwa ambayo mmeweza kuifanya na nimpongeze sama Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya ya maboresho katika bandari. Bado tunahitaji kupunguza muda wa utoaji mizigo pale na kuongeza ufanisi na ikiwezekana bandari yetu iwe inafanya kazi saa 24. Hii iendane sambamba na upanuzi wa Bandari ya Mtwara, ni bandari ambayo inakuja kwa kasi, tukiweza kuwekeza katika Bandari ya Mtwara, hakika kabisa tutakuwa tumepiga hatua kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nichangie, ni ushirikishwaji wa sekta binafsi. Nchi yetu ina sera nzuri sana ya ushirikishaji wa sekta Binafsi (Private Public Partnership) na tuna sheria ambayo inaendana na hiyo sera ambayo tunayo. Katika upande wa utekelezaji tumekuwa na changamoto kubwa sana, sasa nadhani umefika muda muafaka, miradi yote hii, mipango yetu yote hii, hatuwezi tukaifanya kwa hela ya Serikali, tuishirikishe sekta binafsi katika baadhi ya hii miradi ili sasa Serikali ijikite katika ile mipango mingine mahususi, haya mambo mengine tuweke mazingira mazuri ya uwezeshaji ili sekta binafsi iweze nayo kufanya kazi na tuwape support.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto moja ambayo imekuwa ipo ni kwamba Serikali imekuwa na bureaucracy kubwa sana na tumekuwa tunawa-frustrate sana wawekezaji ambao wanataka kuja kushirikiana na sisi Serikali. Kwa hiyo, naomba sana Serikali itengeneze mazingira mazuri ili kwa wawekezaji binafsi tuweze kuwashirikisha kwa kupitia mpango wa PPP.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kuligusia ni eneo la barabara hususani katika Mkoa wa Dar es Salaam. Tumekuwa tunaliongelea sana jambo hili, Dar es Salaam sasa hivi kwa mtu kutoka maeneo anayoishi kuweza kufika mjini si chini ya masaa mawili na masaa mawili tena wanayatumia kutoka katika maofisi kwenda majumbani. Tumekuwa tunaongelea masuala ya barabara ya mzunguko (ring roads). Niiombe sana Serikali ifike sasa wakati tuwekeze na tuwe na dhamira ya dhati kuwekeza katika barabara za mzunguko katika Mkoa wa Dar es Salaam, tuondokane na hii adha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kufanya investment kubwa kwa wakati mmoja, tunaweza tukawa tumeondokana na hili. Tuna miradi mingi ambayo tumeweza kuifanya, tuna Mradi DMDP, lakini tuje na mradi mahususi ambao utaondoa kero ya usafiri katika Mkoa wa Dar es Salaam. Tunashukuru kwa kuona kwamba zile flyovers zimeanza kujengwa, lakini niongelee kwa upande wa mimi kama Mbunge wa Kigamboni, tumejenga daraja, linakamilika mwezi Machi, lakini tuna changamoto ya approach roads kwa upande wa Kigamboni lakini vilevile kwa upande wa Kurasini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili daraja halitakuwa na manufaa iwapo zile approach roads kuanzia Bendera Tatu mpaka Kamata hazitajengwa. Niiombe sana Serikali, tumefanya investment kubwa sana ya over two hundred billion pale katika Daraja la Kigamboni lakini tuhahitaji zile approach roads ili sasa lile daraja liweze kutumika kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kuligusia ni upande wa maji. Inasikitisha kuona kwamba nchi yetu ni asilimia ndogo sana ya wananchi ambao wana huduma ya maji. Ni jambo ambalo nalo tumekuwa tunaliongelea kwa muda mrefu sana, tumeweka mikakati na nakumbuka katika Bunge la mwaka jana au mwaka juzi tuliweka mikakati mahususi na tukatenga bajeti, kwamba, Serikali itumie fedha hii katika kuhakikisha kwamba huduma ya maji tunaisambaza. Naungana mkono na Wabunge wengine ambao wana mtazamo tuwe na Agency kama REA kwa ajili ya maji vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, hii itasaidia sana na tu-specify vyanzo vya mapato ambavyo vitakwenda pale kuhakikisha kwamba kama tulivyokuwa na Mfuko wa Barabara na Mfuko wa Umeme Vijijini, basi tuwe na chanzo cha fedha kwa ajili ya maji vijijini, itatusaidia sana kuweza kupiga hatua katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tena katika eneo hilo la maji, tuna mradi wa maji ya chini kule Kimbiji, Kigamboni, mradi ambao unafadhiliwa na Benki ya Dunia, unachimba visima 20,000. Niwaombe sana, mradi ule unasuasua mno na ni mradi muhimu sana kwa sisi wakazi wa Kigamboni ambao hatuko katika mfumo wa maji salama kwa DAWASA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba mradi ule uharakishwe na usambazaji uweze kufanyika na wanufaika wa kwanza wawe wananchi wa Kigamboni. Hatutakubali maji yale yakaondoka Kigamboni bila wananchi wa Kigamboni kuwa walengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nataka kugusia katika sekta ya afya, tuna changamoto kubwa sana. Burden of disease inazidi kuongezeka, tuna magonjwa ya kuambukizwa na sasa hivi tunaanza kuona magonjwa yasiyoambukizwa, none communicable diseases. Idadi ya wananchi wa Tanzania inaongezeka kwa kasi kubwa sana, sijui kama wachumi wetu na sisi mnakaa mnaliona hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka tunaongeza Watanzania takribani milioni moja, Watanzania hawa wanahitaji huduma za jamii, bajeti ya afya inashuka kila mwaka, sasa hivi tuko kwenye eight to nine percent. Kuna umuhimu sasa wa kuhakikisha kwamba tunakuwa na vyanzo mbadala vya kuendesha sekta ya afya na mimi ni muumini mkubwa sana wa universal coverage, wananchi wote tuwaingize katika mfumo wa bima ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika suala la UKIMWI linatufedhesha sana. Asilimia 90 ya fedha za kuendesha mradi wa UKIMWI nchini zinatoka kwa wafadhili na sasa hivi tuko katika hali ngumu kidogo, wafadhili wametuambia tuweke Matching Funds ambayo sisi hatujaweka. Mwaka jana tumepitisha Sheria ya Aids Trust Fund, ni hatua nzuri, lakini niombe sana twende mbali zaidi ku-specify, kwa sababu mwaka jana tuliweka kwamba tuwe na three hundred billion Serikali haiku-commit hiyo fedha. Kwa hiyo, niiombe sasa twende mbali, tu-identify vyanzo na tuweze kuwa na fedha za kuendesha Mfuko wa UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nashukuru sana na naipongeza Serikali kwa uwasilishaji mzuri. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa nami nichangie katika bajeti kuu. Nianze kwa kusema kwamba kauli mbiu ya bajeti hii naikubali ambayo imelenga kuongeza uzalishaji viwandani na kupanua fursa kwa ajira. Niseme tu kwamba nasi kama Jimbo la Kigamboni tumeshajipanga vizuri, tayari tumeshapima ekari 1,000 na tumetoa viwanja vipatavyo 461 vya viwanda ambavyo viko tayari kwa uwekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile niseme tu kwamba bajeti hii mwelekeo wake ni mzuri, kutoka asilimia 26 mpaka asilimia 40 ya fedha za ndani kutengwa katika kuelekea katika bajeti ya maendeleo, ni jambo jema. Jambo jema lingine ni kupunguza utegemezi kwa wahisani.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna changamoto ambazo nami naziona. Pamoja na juhudi ambazo zinaendelea za kuongeza ukusanyaji wa kodi za ndani, bado tuna changamoto ya wigo wa kukusanya kodi, kwa maana ya tax base, hilo bado ni tatizo kubwa sana. Bado naona tunaendelea kuvikamua vyanzo vile vile ambavyo tumekuwa tunavitumia siku zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kwamba sasa hivi inabidi tuangalie na vyanzo vingine. Sekta ya Kilimo, Uvuvi pamoja na Utalii vinaweza vikachangia kwa kiasi kikubwa. Tuweke pesa ili tupate pesa. Kwa hiyo, nataka kuishauri Serikali ijaribu sasa kuangalia vyanzo vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilikuwa nataka kushauri ni kuhusiana na matumizi makubwa ndani ya Serikali. Tunaziona juhudi ambazo mnazifanya katika kupunguza matumizi ya Serikali. Asilimia 49.5 ya mapato ya ndani yote yanaenda kwenye mishahara. Hii ni gharama kubwa sana. Ni lazima sasa mwangalie upya ndani ya Serikali, kuangalia reforms za kuboresha ufanisi lakini na kupunguza gharama ambazo zinaingia katika masuala ya mshahara.
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tuangalie tena maeneo mengine ambayo tunaweza tukapunguza matumizi makubwa. Katika eneo la ununuzi wa magari, matumizi ya magari ya Serikali bado ni mbovu. Tunayanunua magari kwa gharama kubwa. Ni muda muafaka sasa kuweka sera nzuri ya ununuzi, matumizi na matengenezo ya magari ya Serikali; yanatumia gharama kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka kuchangia ni ushirikishwaji wa sekta binafsi. Tuna Sheria nzuri ya PPP na sera nzuri sana ya PPP; lakini ukiangalia katika hotuba hii ya bajeti kwa kiasi kikubwa sana, miradi yote mikubwa tunategemea sana Serikali kwenda kukopa fedha kwa ajili ya kuendesha hiyo miradi. Kwa nini tusi-engage sekta binafsi tuka-freeup some resources kwa ajili ya huduma nyingine za jamii kama afya, elimu na maji? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishauri Serikali ijaribu kuangalia hii, miradi mingine kuna watu wana fedha zao, tuwashirikishe ili hizo fedha nyingine tuweze kuziokoa kwa ajili ya mambo mengine katika huduma za jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilikuwa nataka kuchangia ni concern. Sisi kama Bunge jukumu letu ni kupitisha bajeti ya Serikali. Nilipokuwa nasoma hotuba ya Kamati ya Bajeti, imenishtusha kidogo kuona kwamba Serikali inatumia fedha kupita kile kiwango ambacho kimeidhinishwa na Bunge, hilo ni kosa. Tuanze sasa kujenga msingi wa Serikali kuheshimu maazimio na zile idhini ambazo zimepitishwa na Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupeleka fedha asilimia 140, 120, 150 zaidi ya zile zilizopitishwa na Bunge bila kuleta maombi hayo Bungeni ni kuvunja sheria na kuvunja Katiba. Kwa hiyo, lazima sasa tufike mahali turudi kwenye ile misingi ya matumizi ya fedha ya Serikali na nidhamu ya matumizi ya fedha za Serikali izingatiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kulichangia ni hususan ushirikishwaji wa Kamati ya Bajeti. Kamati ya Bajeti inafanya kazi kwa niaba ya Bunge. Serikali ione kuwa, wanapofanya kazi na Kamati ya Bajeti, wanafanya kazi na Bunge. Ni muhimu sana wakawashirikisha. Bajeti itakuwa nyepesi kama Kamati ya Bajeti itakuwa imeridhia kwa niaba yetu sisi. Sasa Serikali inapokuwa inaleta bajeti na vitu vingine havijapitishwa katika Kamati ya Bajeti mnaifanya kazi ya kujadili na kupitisha bajeti inakuwa ngumu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali, Bunge linaweza likawa rafiki pale mnapokuwa mnatoa ushirikiano kwa Bunge, lakini kazi inaweza ikawa ngumu pale mnapokuwa hamuwashirikishi Wabunge kikamilifu. Sasa nawaomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, msiwaone Kamati ya Bajeti kwamba wale ni maadui, wale ni marafiki zenu na wako pale kwa niaba yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema, nami nataka kugusa suala la kiinua mgongo kwa Waheshimiwa Wabunge na nataka Mheshimiwa Waziri wa Fedha naye ajaribu kunisaidia, nini hasa lengo la kuiweka hoja hii katika bajeti yake? Kwa sababu Bunge letu hili ndiyo limeanza 2015 litakwisha 2020; unapoliweka hili suala la kukata kodi katika kiinua mgongo, lengo lake ni nini? Ama ilikuwa kama hivyo alivyokuwa anasema Mheshimiwa Kangi Lugola, kuwa-beep Waheshimiwa Wabunge?
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme, huwezi ukaleta usawa katika kupofua wenzako. Kama kuna watu vipofu nawe ukawapofua wengine ili wote tuwe sawa, nadhani hiyo siyo mantiki sahihi. Suala kubwa la msingi hapa, kama tunaongelea masuala ya kiinua mgongo, lets cut across board. We should not single out a single group. Kwa hiyo, hili nataka niliseme kwa Mheshimiwa Waziri ili liweze kueleweka. Maana yake unapokuwa na single out a single group, inaleta mashaka kuhusu dhamira ya lengo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nakushukuru sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MASUALA YA UKIMWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI, napenda kuwashukuru sana wachangiaji wote ambao wamechangia hoja hii, walikuwa wengi sana waliochangia kwa maandishi, lakini vilevile ambao walichangia kwa kuongea. Lakini kwa nafasi ya kipekee nimshukuru sana Waziri wa Sera na Bunge, Mheshimiwa Jenista Mhagama ambaye alishiriki vikao vyetu vyote na kwa ukamilifu kuanzia asubuhi mpaka muda ambao tulikuwa tunamaliza, namshukuru sana na kumpongeza sana.
Vilevile niwapongeze Wajumbe wa Kamati mpya ya UKIMWI kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameifanya kuhakikisha kwamba taarifa hii inakamilika ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kusema kwamba vita dhidi ya masuala ya UKIMWI na vita dhidi ya dawa za kulevya inahitaji dhamira ya dhati. Bila dhamira ya dhati tutakuwa tunapiga porojo na tutakuwa tunaongea lakini vita hii hatutaiweza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisisitize katika maeneo machache na la kwanza nisisitize katika suala la sera. Katika Bunge la Kumi tulifanya mapitio ya Sera ya UKIMWI na Sheria ya UKIMWI lakini vilevile Sheria ya Tume ya Dawa za Kulevya ambazo zilielezea kuhusiana na muundo na mamlaka ambazo sheria hizi zimepewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kwa kusema, kwa kweli Sera ya UKIMWI nayo ni ya muda mrefu, ni ya mwaka 2001 sasa hivi ni mwaka wa 16, tunahitaji tuipitie upya sera ile ili iweze kuendana na mazingira ya sasa. Vivyo hivyo, kuhusiana na Sera ya Dawa za Kulevya ni ya mwaka 2004, mbinu zimebadilika, mahitaji yamebadilika na aina ya dawa za kulevya yamebadilika, tunahitaji sera mpya ambayo itaendana na mazingira ambayo tunayo sasa. Sheria tulizozipitisha zimeelekeza kuhusu muundo mpya, tuiombe Serikali, ili kama tuna dhamira ya dhati katika vita hii, basi miundo hii ya hizi taasisi ambazo zimeundwa upya kisheria basi ziweze kufanya kazi ikiwa ni pamoja na kupewa watumishi ambao wanahitajika kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo nataka nigusie ni suala la fedha, taasisi zote mbili. Tumeanzisha Mfuko wa Masuala ya UKIMWI, ni jambo jema, Serikali iliahidi shilingi bilioni tano imetoa shilingi bilioni 1.5, mahitaji ya masuala ya UKIMWI kwa mwaka ni takribani shilingi trilioni 1.3, hivi sasa fedha ambazo zinapatikana katika masuala ya UKIMWI ni shilingi bilioni 800, tuna gap ya takribani shilingi bilioni 500, tunahitaji tuongeze nguvu zaidi. Fedha za wafadhili zinapungua, ni lazima sasa tujielekeze katika vyanzo vya ndani. Niiombe Serikali na Waheshimiwa Wabunge wote kwa pamoja, ni muda muafaka sasa kuungana, tuhakikishe katika bajeti inayokuja Serikali ije, au sisi kama Wabunge tupendekeze vyanzo mahsusi, kama ilivyokuwa katika Mfuko wa Barabara, kama Mfuko wa Mawasiliano na Mfuko wa Elimu, sasa tuwe na source maalum kwa ajili ya kuwezesha shughuli za UKIMWI. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono kauli ya Mheshimiwa Rais leo asubuhi. Katika Kamati yetu na kama mtasoma katika mapendekezo yetu, tulikuwa tunataka kauli za viongozi wa Kitaifa kukiri kwamba suala la dawa za kulevya ni janga, na leo asubuhi Mheshimiwa Rais ameitamka hiyo kauli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, na mimi niwaombe viongozi wengine, tuendelee kuibeba kauli ya Mheshimiwa Rais na sisi twende tukayasemee. Ndugu zangu, UKIMWI ulipoanza mwaka 1979 tulisema UKIMWI ni tatizo la sehemu fulani katika Tanzania yetu, hivi tuvyoongea hakuna familia ambayo haijaguswa. Na ninyi mtakuwa mashahidi, katika vijiji vyetu, vitongoji vyetu katika Wilaya zetu na Majimbo yetu, tuna wagonjwa ama tuna watu ambao wanatumia dawa za kulevya na waathirika wa dawa za kulevya. Tunapokwenda ni kubaya zaidi, tunahitaji tuweke nguvu sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu na sisi tungependa kusisitiza; tuna Kamati zetu katika halmashauri ambazo zinasimamia masuala ya UKIMWI na sisi kama Wabunge ni wajumbe wa zile Kamati za UKIMWI. Tunapendekeza na tungewaomba Serikali na hili mliwekee msisitizo, zile Kamati zipewe majukumu ya ziada ya kuwa ni Kamati za Halmashauri kusimamia masuala ya UKIMWI na dawa za kulevya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Kamati tunaunga mkono suala la viroba linaharibu vijana wetu, linaharibu kizazi chetu, linaharibu Taifa letu. Tanzania tunapoelekea sasa hivi tunakuwa ni Taifa la watu walevi, na bahati mbaya sana tumezi-package hizi pombe kwa kiwango cha chini sana. Leo nilikuwa naongea na Mheshimiwa Mbunge mmoja anasema kule Kanda ya Magharibi pombe hizi zinauzwa shilingi 300, mpaka watoto wadogo ambao wanapewa nauli ya kwenda shuleni wana uwezo kununua ile pombe. Sasa niiombe Serikali, kwa kweli kama ni mapato yote yanapatikana kwa njia hii haramu haiwezekani, tupige vita viroba na sisi kama Wabunge tutawaunga mkono ili tuondokane na hili janga tuweze kujenga kizazi imara kwa miaka ijayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamegusia suala la tohara; ni kweli katika suala la kitaalam ni intervention ambayo imeonekana inaweza ikasaidia katika kupunguza ugonjwa ya UKIMWI, ni kitu ambacho kimekuwa proven. Lakini hatuwezi tukalazimisha mtu akafanye tohara, muhimu tuwekeze katika elimu na watu waelewe umuhimu na faida ambazo wanaweza kuzipata kutokana na jambo hili, naamini hilo tukiweza itatusaidia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna changamoto kubwa sana; tumetoa elimu, na tuliwekeza sana katika elimu ya UKIMWI lakini inaonekana bado tuna changamoto kubwa. Maambukizi kwa vijana kati ya miaka 15 mpaka 19 ni makubwa sana, kwa mujibu wa takwimu ambazo zimetoka hivi karibuni za Tanzania Demographic Health Survey zinaonesha…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniruhusu kuendelea. Nilikuwa nasema kwamba, katika rika la vijana wa miaka 15 mpaka 16, hususan kwa wasichana, asilimia 27 wameshapata ujauzito. Sasa tunahitaji kwa kweli tuwekeze nguvu kubwa sana katika rika hili kupunguza mimba za utotoni, lakini vilevile katika kupunguza maambukizi. Na hili suala la elimu naomba sana, tunahitaji sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge tujielekeze huko, lakini vilevile katika jamii nzima kuhakikisha kwamba jamii na sisi kama wadau tunashiriki katika kuwajenga vizuri kimaadili watoto wetu, lakini vilevile kuwapa elimu jinsi ya kujikinga na maambukizi ya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kuligusia ni hususan katika upande wa dawa za kulevya, kuna intervention ama mkakati ambao unasaidia kupunguza athari kwa wagonjwa ambao wanatumia dawa za kulevya. Niseme jambo moja ambalo limeongelewa hapa, watumiaji wa dawa za kulevya sio vichaa, na watumiaji wa dawa za kulevya sio wahalifu na hawapaswi kuwekwa jela, ni watu ambao wanahitaji kupata msaada wa tiba na magereza sio sehemu yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuwatia moyo, tumeipiga vita na baadhi nimesikia ni maneno yapo ya kupiga vita sober houses, hatuhitaji kupiga vita sober houses, tunahitaji kuziboresha kuwasaidia na kuzisimamia na kuziratibu. Lakini vilevile Serikali iongeze nguvu kuhakikisha kwamba tuna rehabilitation center yetu ambayo tumekuwa tunaijenga pale Dodoma na tuliliongea hilo, Serikali iweke msukumo tuimalize ile pale. Watumiaji wa dawa za kulevya wasiwekwe Isanga ili sasa wawekwe kule wakapate tiba, wapate msaada wanaohitaji ili warudi katika jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwashauri Waheshimiwa Wabunge maana yake na mimi nasoma kwenye mitandano na magazeti, kutoka katika dawa za kulevya sio shughuli ndogo. Ni sawasawa na huyu ambaye anatumia sigara, kuna mwingine anaweza akaacha papo kwa papo, lakini kuna wengine wanaweza wakachukua hata miaka mitano; anaingia, anatoka, anaingia anatoka. Wanahitaji msaada mkubwa sana badala ya kuwanyanyapaa tuwasaidie waweze kurudi kwenye mstari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na niokoe muda wako, nishukuru, mapendekezo yetu tumeyatoa na tumeyatoa kwa kirefu sana. Niombe sana Serikali ijaribu kuzingatia ili tutakapokutana tena katika Kamati basi itupe mrejesho wametekeleza kwa kiasi gani na wapi wamekwama na kiasi gani wamekwama ili na sisi kama Kamati ya Bunge ambayo inasimamia suala hili tuweze kutoa na kushauri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nakushukuru sana kwa kunipa fursa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nitoe hoja kwamba yale mapendekezo ambayo tumetoa kupitia katika taarifa yetu yaweze kupokelewa na kufanyiwa kazi na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi kwa rehema yako kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu ili niweze kuta hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Katika kipindi hiki cha utendaji wa kazi nikiwa kama Naibu Waziri nimepata ushirikiano mkubwa kutoka kwa viongozi na wafanyakazi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Shukurani za pekee kabisa nazielekeza kwa Mheshimiwa Dkt. Ummy Mwalimu namuita daktari, Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa ujuzi wake na ubobezi katika sekta ya afya na kwa ushirikianoa ambao amenipa katika kutkeleza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha napenda kuwashukuru Makatibu Wakuu Dkt. Mpoki Ulisubisya pamoja na Sihaba Nkinga kwa mchango wao kwa kuwezesha utekelezaji wa majukumu yangu. Vilevile nawashukuru Profesa Mohamed Bakari - Mganga Mkuu wa Serikali, na pia nachukua fursa hii kuwashukuru watendaji wa wizara taasisi za Wizara pamoja na Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Waganga Wafawidhi wa Hospitali, Vituo vya Afya na Zahanati; Vyuo vya Mafunzo vilivyo chini ya Wizara yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile natoa shukurani zangu kwa ushirikiano ambao wameendelea kutupa katika sekta ya afya maendeleo ya jamii na ustawi wa jamii na wananchi wote kwa ushirikiano.

Mwisho natoa shukurani zangu za dhati kwa watoa huduma wote katika sekta ya afya kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuitoa na uzalendo wao. Sifa tunazipata sisi Mawaziri lakini kazi kubwa zinafanyika huko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze katika kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge na la kwanza nitajiekeza katika hoja ambazo Wabunge wengi wamechangia kuhusiana na masuala ya miundombinu katika sekta ya afya. Serikali imekuwa inafanya kazi kubwa sana kuboresha zahanati, vituo vya afya na hospitali kwa mujibu wa Mpango wetu wa Maendeleo ya Afya ya Msingi ambapo zinaelezea kwamba kila kijiji kitakuwa na zahanati na kila kata itakuwa na kituo cha afya. Tumeboresha kwa kiasi kikubwa sana vituo vya afya na Waheshimiwa Wabunge wengi humu ndani mtakuwa mashuhuda kwamba vituo vingi vya sasa hivi vimeboresha, zaidi 208 .

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya TAMISEMI ambayo tumeipitisha hivi karibuni tumesema kwamba tutajenga Hospitali za Wilaya 67; katika mapendekezo ambayo tunaleta katika Bunge lako tukufu hili baada ya Serikali kutukabidhi Hospitali za Rufaa za Mikoa tutaanza ujenzi wa hospitali sita za rufaa za mikoa pamoja na kuboresha hopsitali nyingine za rufaa katika maeneo ya afya ya mama, mtoto na huduma za dharura. Kwa hiyo, tumeendelea pamoja na hilo kuboresha huduma mbalimbali katika Hospitali zetu za Kikanda, Hospitali zetu Maalum na Hospitali za Rufaa za Muhimbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambasamba na kuboresha masuala ya miundombinu tumejielekeza katika kuboresha ubora wa huduma za afya. Moja ya jambo ambalo tumeweza kulifanya kama Serikali ni kuanzisha mfumo wa star rating ambao unaweka viwango vya ubora katika utoaji wa huduma na kwa kiasi kikubwa tumeweza kufanikiwa sana. Tuliweza kufanya tathimini ya awali ambapo zaidi ya asilimia 33 ya vituo vya kutoa huduma ya afya vilikuwa na viwango vya nyota sifuri; lakini baada ya kuja kufanya tathimini na maboresho makubwa viwango vile vimepungua sna kwenda chini ya asilimia 10 ni mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunaka tujielekeze zaidi kwenda mbali zaidi, tutatoa viwango vya ubora katika utoaji huduma. Sambasamba na hilo tunataka tuanzishe utaratibu wa kutoa leseni kwa vituo vyetu vya utoaji huduma vya afya ambavyo sasa badala mtu kuwa kutoa huduma tu pasipokuwa na kuzingatia viwango vya ubora tutaanza kutoa leseni na leseni hii inahuishwa na viwango vya ubora ambavyo anavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ambayo iliibuka kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge ni kwamba ni nani mwenye mamlaka ya kupandisha hadhi vituo vya afya na zahanati. Niseme tu, kwa mujibu wa instrument tuliyo nayo Wizara ya Afya ndio mamlaka pekee ambayo ina mamlaka kisheria ya kupandisha hadhi zahanati na vituo vya afya; na hii inaendana sambamba kabisa na majukumu ambayo Wizara ya Afya inayo. Wizara ya Afya itasimamia sera, masuala yote ya viwango na miongozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Wizara ya Afya itasimamia Wizara zote za Rufaa za Mikoa, Hospitali za Kanda, Hospitali Maalum na Hospitali za Taifa. Wenzetu Ofisi ya Rais, TAMISEMI majukumu yao ni kusimamia utekelezaji wa sera, viwango na miongozo inayotolewa na Wizara ya Afya, lakini sambamba na hilo watasimamia Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya; huo ndio mgawanyo wa majukumu ambao tunao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kidogo katika suala la dawa, na hoja zimekuwepo nyingi na Waheshimiwa Wabunge wamechangia sana. Niseme tu kwamba katika awamu hii ya tano bajeti ya dawa imeongezeka kutoka bilioni 31 mwaka 2015/2016 kufika bilioni 269 katika mwaka huu wa fedha na mwakani tutakuwa na bilioni 270. Tumekwenda mbali zaidi kuimarisha mifumo yetu, takribani kama wiki tatu/nne tulikuwa tunazindua magari mapya 181, na mfumo ambao tunautumia ni kuhakikisha kwamba dawa tunazipeleka mpaka katika kituo cha kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambasamba na hilo tumeweka mwongozo wa utoaji wa huduma na hili nilitaka nilisisitize. Tumeweka mwongozo wa kutoa huduma za afya za dawa, tunasema dawa gani itatolewa wapi kwa ngazi gani kwa ugonjwa gani. Kwa sababu tulikuwa tunapata changamoto katika hospitali kubwa kwamba kampuni za dawa zilikuwa zinaenda kwa watoa huduma, wanawaambia andika dawa hii na utakapokuwa umeandika dawa hii ikawa inanunuliwa kwa wingi na sisi tutakuwa tunakupa commission. Na hii wakati ikasababisha zile dawa zisiwe zinapatikana pale kwa sababu tu wale wafanyabiashara walikuwa ndio wanatoa mwongozo wa jinsi gani ya dawa kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tumeweka mwongozo wa kutoa dawa ambao sasa utatoa mwongozo dawa gani inatumika wapi na katika aina gani ya ugonjwa. Lakini sambamba na hilo, tumekwenda mbali kuweka label katika dawa zetu. Kwa hiyo, ninaamini mifumo hii ambayo tunaendelea kuiboresha itahakikisha kwamba dawa tunazipata kwa kiasi cha kutosha. Hata hivyo nitoe rai, na kwa Waheshimiwa Wabunge kwa sababu wengi wameniuliza mbona dawa fulani haipatikani. Kuna dawa zipo katika ngazi tofauti tofauti, hatutegemei tukakuta dawa kwa mfano insulin katika zahanati, hatuwezi tukazikuta zile. Zile dawa ziko katika ngazi tofauti kwa sababu dawa zile zinategemea na aina ya utaalam ya wale ambao wanatakiwa kuzitoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunatambua kwamba magonjwa yasiyoambukizwa yanazidi kuongezeka na sisi tutakuwa tunapitia miongozo yetu mara kwa mara kuangalia wapi tunahitaji kuboresha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuja na hoja nyingine ya masuala ya CT Scan na MRI katika hospitali za Rufaa za Mikoa. Kwa sasa hivi kwa mujibu wa miongozo yetu, huduma hizi haziwezi zikapatikana katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. Ngazi ambazo CT Scan na MRI zinaweza zikaanzia, kwa mujibu wa miongozo yetu ni katika ngazi ya Rufaa za Kanda. Hata hivyo kadri nchi yetu inavyozidi kuongezeka na huduma zinazidi kuboreshwa tutafanya mapitio kuangalia kama tunaweza sasa tukaruhusu teknolojia hizi zikaweza kutumika katika ngazi hii kwa sababu changamoto hii si suala tu la kuwa na vifaa hivi ni suala vilevile kuwa na wataalam ambao wanaweza kusimamia vifaa hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lilikuwa ni suala la rasilimali watu. Tunakiri kwamba tumekuwa na changamoto kubwa ya rasilimali watu na nimshukuru sana Mheshimiwa Mkuchika, ameainisha vizuri sana kwamba katika mgao utakaokuja na sisi tutapata mgao katika watumishi wa afya. Naamini katika hili litatusaidia sana kupunguza changamoto ya watumishi ambayo tunayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo lilikuwa limeongelewa na hili nataka niwapongeze watoa huduma kwa kweli kwa kiasi kikubwa sana, kelele za wananchi kuhusu utoaji wa huduma zimepungua sana. Lugha za matusi na masuala ya rushwa kwa watumishi wa afya tumepunguza sana; na hii niwashukuru sana na kuyapongeza mabaraza ya kitaaluma na maadili ambayo yako chini ya Wizara ya Afya. Tumezidi kuyaboresha na tumeendelea kuhakikisha kwamba tunafanya mabadiliko ya kisheria kuhakikisha kwamba taaluma hizi tunazisimamia vizuri. Moja ya mikakati ambayo tumeiweka ni kuhakikisha kwamba sasa kada zetu zote tunatoa leseni.

Mheshimiwa Naibu Spika, msije mkashangaa, tumepitisha Sheria ya Madaktari ambayo itahitaji hata mimi Naibu Waziri ambaye nimesimama hapa ni daktari, baada ya muda mtakuwa na mimi mnaniona dispensary pale natoa huduma au Hospitali ya Benjamin Mkapa ili kuhakikisha kwamba tunapata mafunzo endelevu kuhakikisha kwamba na mimi ili niendelee kuitwa daktari na ku-practice kama daktari ninakuwa na leseni yangu na ninapata mafunzo endelevu na yote hii ni mikakati ya Serikali kuhakikisha kwamba watoa huduma wote wanakuwa… muda umekwisha?

NAIBU SPIKA: Endelea.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze sasa katika ngazi ya maendeleo ya jamii. Kuna hoja kama mbili/tatu ambazo nazo ziligusiwa sana na Waheshimiwa Wabunge na moja lilikuwa suala la NGO’s, kwamba kuna NGO’s nyingi hapa nchini. Nyingi ni NGO za Kimataifa lakini zimejisajili kama NGO za hapa nchini. Sambamba na hilo kuna fedha nyingi ambazo zinakuja kwenye NGOs na hazijulikani zinakwenda wapi. Tatu, ilikuwa ni kwamba kuna baadhi ya NGO’s zimekiuka majukumu yao ya kikatiba na kuanza kujiingiza katika mambo mengine ikiwa ni pamoja na siasa.

MheshimiwaNaibu Spika, kupitia idara yetu ya NGO tumefanya tathmini ya NGOs zote, kuangalia usajili wao, kuangalia mifumo yao ya fedha, kuangalia wanafanya shughuli gani, kuangalia kama je wanawasilisha taarifa muhimu zote ambazo zinatakiwa kwa mujibu wa sheria na tumekuta NGOs nyingi ambazo zimekuwa zinakiuka masharti haya na baadhi tumeshazifuta na nyingine zimepewa maonyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tumewekeza nguvu kubwa sana kuhakikisha kwamba sasa tunazisimamia vizuri hizi NGOs ili ziweze kutimiza majukumu yake. Hatuna shida na NGO’s; ni wadau wakubwa sana wa Serikali na sisi kama Serikali tuna-appreciate sana kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine la mwisho ambalo nilitaka nigusie lilikuwa ni suala la wazee. Sisi kama Serikali kupitia Sera ya Afya ya mwaka 2007 tunatambua umuhimu wa wazee na katika sera yetu imesema kwamba wazee watapewa matibabu bure. Mheshimiwa Waziri amekuwa kinara katika hili kuhakikisha kwamba tunatenga madirisha ya wazee na wazee wetu wanapata vitambulisho vya kuweza kuwatambua na kuweza kupata matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakiri kwamba tumekuwa na changamoto kidogo katika utekelezaji wa hili, lakini na sisi tutaongeza juhudi zaidi kuhakikisha kwamba tunasimamia kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, imekuja hoja ambayo ilikuwa raised hapa kuhusiana na Sheria ya Wazee. Tuna Sera ya Wazee ya mwaka 2003, sasa hivi tunaifanyia mapitio na baada ya hapo tutaileta kwa ajili ya kuleta hiyo rasimu ya sheria ili iendane na mazingira ya sasa ya hali ya wazee tuliokuwa nao hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, mimi nikushukuru sana na niwashukuru watoa hoja wote kwa michango mizuri ambayo wameweza kuitoa katika bajeti yetu. Sisi tunaamini kwamba michango hii itatusaidia sana kuboresha utendaji wetu wa kazi. Nawashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kuwepo katika Bunge lako Tukufu na kuweza kuchangia hoja iliyowasilishwa hapa Bungeni tarehe 07 Mei.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa njia ya pekee kabisa naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kutumikia nafasi hii ya Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Aidha, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa kwa maelekezo mbalimbali ambayo ameendelea kutupatia katika utekelezaji wa majukumu yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa njia ya kipee kabisa napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, mimi namwita Daktari kwa ushirikiano wake wa hali ya juu sana na miongozo mbalimbali ambayo ameendelea kunipatia katika utekelezaji wa majukumu. Amekuwa ni nguzo moja muhimu sana na mafanikio haya tunayapata ni kwa sababu ya uongozi wake mahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa michango yao, maoni yao na ushauri wao kwa kiasi kikubwa sana wamekuwa ni dira na miongozo wetu na tunaahidi kwamba tutazingatia maoni na ushauri wao katika kutekeleza majukumu yetu ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru timu ya wataalam ambao na sisi tunawaongoza, Makatibu Wakuu wawili, Dkt. Zainabu Chaula, Katibu Mkuu wa Fungu 52 na Dkt. John Jingu wa Fungu 53 kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Kazi nzuri inaonekana kwa sababu na kazi nzuri ambayo wao kama Makatibu Wakuu na Watendaji wote wameendelea kuifanya pamoja na Wakuu wa Taasisi, vyuo vya mafunzo na hospitali zetu zote ambazo na sisi kama Wizara tunazisimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini haya yote yasingeweza kwenda vizuri kama nisingepata support ya wale wananchi ambao wamenileta hapa, wananchi wa Kigamboni na naomba nitambulishe pale juu gallery leo nina viongozi wa Chama cha Mapinduzi natumaini utapata fursa ya kuwatambua kutoka Wilaya ya Kigamboni na Waheshimiwa Madiwani wote kutoka Wilaya ya Kigamboni nao wapo hapa kuja kushuhudia wasilisho la hotuba hii. Niendelee kusema kwamba Kigamboni tunawakilisha vizuri ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache sasa naomba nijielekeze katika baadhi ya hoja za msingi ambazo ziliweza kutolewa na Waheshimiwa Wabugne na nianze na hoja za Fungu 53, Fungu la Maendeleo ya Jamii. Niseme tu kwamba moja ya hoja ya msingi ambayo ilijadiliwa sana na Wabunge wengi ni suala la wazee, na suala la wazee sisi kama Serikali tunapaswa tujivunie sana. Katika moja ya mafanikio ambayo Serikali hii imeweza kufanya ni kuhakikisha kwamba umri wa Mtanzania kuishi umezidi kuongezeka, hivi tunavyoongea wastani wa Mtanzania kuishi ni miaka 64.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, maana yake ni nini, ni kwamba ni mafanikio ya mikakati yetu ya lishe lakini mafanikio ya vilevile ya mkakati yetu ya kuhakikisha kwamba Watanzania hawa tunapata huduma nzuri za afya, na ndiyo maana tuna kundi kubwa la wazee ambalo lipo na tunatarajia kwamba kwa hali tuliyokuwa nayo watu wengi watafika zaidi ya miaka 60 ya umri wakiwa na afya njema na kuweza bado wakiwa na nguvu ya kuendelea kutumikia nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Sera ya Wazee ya Mwaka 2003, tunayo na tunaamini baada na sisi kuingalia tumeiona kwamba tunahitaji tuifanyie maboresho na kuja mkakati sasa ambao utakwenda kutibu baadhi ya changamoto hizi za wazee. Lakini naomba niseme kitu kimoja, Serikali inatambua na kuthamini mchango wa wazee ndani ya Taifa letu, na ndiyo maana sisi kama Serikali tuna makazi 17 ya wazee ndani ya nchi lakini tunawahudumia takribani wazee 510 ndani ya makazi haya 17. Utaratibu uliokuwepo ni mmoja; sisi kama Serikali tunawachukua wale wazee ambao kwanza hawana watoto wa kuweza kuwahudumia, na kama wale wazee hawana watoto basi tunajaribu kuangalia, je, wazee hawa hawana ndugu wa kuwahudumia, na je, kama hawa wazee hawana ndugu wa kuhudumia, je, jamii haiwezi ikabeba jukumu hilo. Kama katika vigezo vyote hivi vitatu havipo basi sisi Serikali tunawachukua wale wazee na tunawagharamia kwa vitu vyote, malazi, makazi na mavazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema idadi ambayo ya wazee ambayo tunayo ni takribani 510 na wazee hawa tunawapa huduma hizo zote za msingi na katika jambo ambalo tunalihakikisha Wizara ni kuhakikisha kwamba, hawa wazee wanapata chakula, malazi na mavazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo tumeendelea kuhamasisha halmashauri kuzingatia agizo la Serikali la kuwapatia wazee vitambulisho kwa ajili ya matibabu ili wazee wapate matibabu kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2017 ambayo inasema wazee watapata matibabu bure. Lakini tulienda mbali zaidi na kuhakikisha kwamba hospitali zetu zote zinakuwa na dirisha la wazee, ili wazee wakifika pale waweze kupata matibabu bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sera mpya ya afya ambayo tunayo sasa hivi, tunataka sasa tuende mbali kuona kwamba kuna suala zima la matibabu ya magonjwa ya wazee, kwa sababu wazee hawa kadri kundi linavyozidi kubwa wanakuwa na magonjwa yao ambayo ni mahsusi, geriatric Medicine kwa lugha ya kitaalam nayo tumeshaliona tunaliwekea mkakati ili kuhakikisha kwamba hawa wazee nao tunaweza kuwahudumia vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja katika jambo ambalo Mheshimiwa Waziri aliliongea katika hotuba yake, ni pamoja na haya magonjwa sugu ya non communicable disease ambayo tumeona kweli changamoto na mara nyingi wakienda katika hospitali, dawa nyingi wanazokosa ni zile dawa za pressure, za kisukari na nini, hilo tumeliona na ndiyo maana tumeazimia kama tulivyokuwa tuna mapambano na magonjwa mengine kama kifua kikuu, TB na malaria, tunataka tuanzishe Mpango wa Taifa wa Magonjwa Yasiyoambukiza na ambayo sasa yatakwenda kushuka mpaka katika ngazi ya chini ili huduma hizi za msingi za huduma za matibabu utambuzi, matibabu na tiba ya magonjwa yasiyoambukiza iweze kupatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala jingine ambalo nilikuwa nataka kuligusia ni suala la NGO’S, asas zisizokuwa za Kiserikali. Hivi karibuni tulibadilisha Kanuni, mara nyingi tunatambua mchango mkubwa sana wa Mashirika yasiyo ya kiraia katika kuleta maendeleo na kutusimamia kama sisi Serikali, na tunathamini, tunatambua mchango wao. lakini hivyo hivyo kama walivyotaka kutusimamia sisi na kutaka kupata uwazi na uwajibikaji na sisi tunataka tupate uwazi na uwajibikaji katika taasisi zisizo za kiserikali. Ndiyo maana tumebadilisha Kanuni ili sasa kuwepo na uwazi katika fedha ambazo wanazozipata, lakini uwazi katika uwajibikaji katika yale maeneo ambayo walisema wanaenda kuyafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na changamoto kuna baadhi ya NGO’s zimepata fedha nyingi sana, lakini haziendi katika malengo yale ambayo yalikuwa yanakusudiwa. Na baadhi ya NGO’s zimetoka katika malengo na makusudio ambayo yalikuwa yanayafanya, wameenda kujiingiza katika mambo mengine. Wengine wanapata dola milioni 100 lakini zinazofika kwa walengwa ni chini ya dola milioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeweka utaratibu kwamba fedha zote zinazoingia lazima tuzijue, zinaenda kufanya kazi wapi, lakini tunataka tulete uwiano kwamba kuna baadhi ya maeneo ndani ya nchi yetu huku, zimekuwa na NGO’s nyingi sana lakini kuna maeneo ndani ya nchi yetu hazina NGO’s hata moja na kote huko kuna Watanzania. Sasa tunataka tuweke utaratibu mzuri, tumeanzisha Kanzi data, tuna NGO’s karibuni 9,000 ndani ya nchi yetu, mpaka sasa hivi tumeshaziingiza kwenye Database NGO’s takribani 6,000, tunaendelea na usajili na lengo ni kusudio ni kwamba kila mmoja kule kule alipo hahitaji kuja Dodoma. Tunaweza tukapata taarifa zake tukajua yuko wapi, anafanya nini na fedha alizokuwa nazo kiasi gani, anawajibika kwa utaratibu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niendelee kuwatoa shaka ndugu zangu lengo siyo baya, lengo ni kuweka uwajibikaji na uwazi ili kabisa kuhakikisha kwamba hizi NGO’s ambazo na sisi kama Serikali tunatambua mchango wao ili waweze kufanya kazi zao vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo liligusiwa na Waheshimiwa Wabunge ni masuala ya Mitaala ya Vyuo vyetu vya Maendeleo ya Jamii na Vyuo vya Ustawi wa Jamii, haya Waheshimiwa Wabunge tumeyapokea, tutaenda fanyia kazi ili sasa Mitaala hii iendane na mazingira ya sasa na uhitaji wa sasa wa Tanzania ambayo tunaelekea katika Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika maeneo mengine ya Sekta ya Afya hususan Vote 52. Namshukuru sana Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI amegusia suala la watumishi, rasilimali watu. Na mimi niendelee kuongezea kidogo tu katika hili, pamoja na changamoto hii tuliyokuwanayo ya rasilimali watu, sisi kama Wizara ya Afya hatujakaa tukalala. Tumeangalia ubunifu ambao tunaweza tukatumia kuangalia jinsi gani tunaweza kutumia rasilimali chache, watu hawa tuliokuwa nao ili kuweza kuleta tija katika utoaji huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya jukumu ambayo tumeweza kulifanya katika lugha ya kitaalam wanaita task shifting, kwa sababu unaweza ukaenda katika kituo cha afya, daktari yule, kwa mafunzo ambayo tunayo, mimi ninaweza nikachoma sindano, nikafunga kidonda na ninaweza nikatoa dawa. Sasa inawezekana mtu akawa pale amemaliza majukumu yake, anaweza akaenda akafanya jukumu lingine ambapo ndani ya kituo. Tumeona tuweze ku- reorient haya majukumu ili basi huduma kwa mwananchi iweze kutolewa, kwa sababu wataalam wengi wa afya tumeweza kupata mafunzo katika nyanja mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tumeanza kutumia wataalam wengine ambao sio wataalam wa afya, wamepata orientation, kwa mfano kwa masuala ya upimaji na uchukuaji wa vipimo. Wameweza kupata orientation na wanaweza wakafanya hayo majukumu. Tunataka tufanye orientation ya Maafisa Maendeleo ya Jamii, Maafisa Ustawi wa Jamii, basi nao waweze kutusaidia kutoa huduma katika baadhi ya maeneo ambayo tunaona yana tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeanza kutumia elimu mtandano (telemedicine). Kwa sasa hivi tunafunga mashine za digitali, dunia nzima ilishatoka huko. Sasa hivi Marekani X- Ray zinasomwa Australia ama inasomwa India. Nasi kwa nini wataalam wetu hawa wachache; na tumeshaanza, pale MOI na Muhimbili tunafunga mashine za kisasa, kutakuwa na screen ziko pale. Mashine zote hizi za X-Ray ambazo tunazifunga Tanzania nzima, itakuwa picha zake zote zinapelekwa Muhimbili na MOI zinasomwa na ndani ya dakika 15 au 20, mtu wa Tunduma, Ruvuma, Mbinga anaweza akapata majibu yake yamesomwa na wataalam. Hizi ni baadhi ya innovation ambazo tunaendelea kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Madaktari wetu Bingwa hawa wachache tuliokuwa nao, tumesema pamoja na kwamba wako katika maeneo ya mjini na katika hospitali zetu kubwa, nami nashukuru sana Hospitali zetu za JKCI, Bugando, MOI, Mloganzila na KCMC wamekuwa wanatoa wataalam wao, wamekuwa wanaenda katika kambi mbalimbali mikoani, wanaendesha kambi za muda mrefu ili wale wananchi wa kule nao waweze kupata huduma hizi za kibingwa na zimekuwa na mchango mkubwa sana na tutaendelea na utaratibu huu kuhakikisha kwamba huduma za kibingwa nazo zinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, innovation tunazo nyingi na ndiyo maana unaona kwamba pamoja na changamoto tulizokuwanazo, hali ya utoaji huduma za afya bado zinaendelea kwa ubora ule ule ambao upo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilitukabidhi Hospitali za Rufaa za Mikoa, nasi tunaendelea kuzipanga. Mkakati wetu wa kwanza ni kuhakikisha kwamba hizi Hospitali za Rufaa katika mikoa ambayo hatuna, ni Hospitali za Rufaa za Mikoa ndiyo tunataka kuanza nazo; Mkoa wa Songwe, Njombe, Geita, Katavi na Simiyu. Ndiyo maana tumeweka nguvu kubwa sana katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya pili tunataka sasa katika maeneo ambayo tayari kulikuwa kuna majengo kwa maana ya Mikoa ya Singida, Tanga kule na Shinyanga, tunawekeza nguvu yale majengo yaanze kupata matumizi lakini awamu ya tatu sasa tutajielekeza katika hizi RRH nyingine kuhakikisha kwamba zile huduma za msingi nazo zinaweza kupatikana ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vifaa na rasilimali watu. Tumewekeza sana sasa hivi katika mafunzo ya wataalam wa afya ili kuhakikisha sasa zile huduma za kibingwa na Madaktari Bingwa wanaweza kupatikana katika maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naamini katika mwaka wa fedha peke yake tumepata kama shilingi bilioni
1.5 kufundisha wataalam zaidi ya 300 na tunataka kwenda mbali. Katika moja ya jambo ambalo tunalitafakari sasa hivi ni kubadilisha mfumo wetu wa mafunzo kwenda kwa utaratibu wa fellowship. Badala ya watu kukaa darasani, watu wanaweza wakaendelea kutoa huduma kule kule tukawapima zile competence zao ambazo tunazitaka na kuwatambua kwamba hawa ni Madaktari Bingwa. Wenzetu wameshapiga hatua kubwa sana katika utaratibu huu, nasi tunaamini ndani ya muda mfupi sisi kama Wizara tutakuwa tumepiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na mambo makubwa mawili au matatu kabla sijarudishia Wizara hii, kuna hoja ilikuja hapa kuhusiana na chanjo ya Malaria. Kwa nini wenzetu wa Malawi wamekuwa na chanjo ya Malaria na kwa nini sisi Tanzania tusianzishe chanjo ya Malaria?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe maelezo ya kitaalam kidogo kwamba mpaka sasa hivi hakuna chanjo ya Malaria ambayo imethibitika asilimia 100 kutoa kinga dhidi ya Malaria. Chanjo nyingi tulizokuwa nazo hapa zinacheza kati ya asilimia 20 mpaka 40. Hamna chanjo ambayo imezidi zaidi ya hapo. Kwa hiyo, chanjo nyingi bado zipo katika ngazi ya hatua ya utafiti na naomba niseme kwamba Tanzania tuko vizuri sana katika masuala ya utafiti wa Malaria. Taasisi yetu ya NIMR inafanya kazi nzuri sana ya utafiti na Taasisi zetu za Ifakara Institute nayo inafanya kazi nzuri sana. Pale tutakapobaini kwamba kuna chanjo ambayo inaweza ikawa ina tija, basi na sisi kama Tanzania tutakuwa ni wa kwanza ku-adopt hizo chanjo kwa ajili ya kuwakinga wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kusema kwamba uwepo wa chanjo hauondi dhana ya sisi kuendelea na mikakati mingine yoyote ya kujikinga dhidi ya ugonjwa wa Malaria. Kwa hiyo, tuendelee kwa sababu mazalia haya haya ya mbu ndiyo hayo hayo mazalia ya ugonjwa wa Dengue, Zika, Kichungunya na magonjwa mengi sana ambayo yapo. Kwa hiyo, nami nataka niwaombe Watanzania tuendelee na mikakati yetu mingine, tunapiga hatua katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria lakini tunahitaji tuongeze kasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, chanjo ya gonjwa la ini, tuna tatizo la ugonjwa wa ini ndani ya nchi. Chanjo ya ugonjwa wa ini tunatoa kwa watoto wote chini ya miaka mitano, ni sehemu ya chanjo ambayo tunaitoa na kwa watu wazima tumekuwa tunatoa kwa wale ambao wako kwenye risk zaidi ikiwa ni pamoja na wataalam wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu ambao tutakwenda nao na tulishakubaliana na Mheshimiwa Waziri ni kwamba kwa yule atakayekuwa anahitaji, tutaweka utaratibu wa chanjo hizi kupatikana kwa gharama nafuu ili mtu mwingine atakayekuwa anajisikia, basi aweze kuchanja kama nasi Waheshimiwa Wabunge tulipata fursa ya kuweza kuchanjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa naomba niongelee suala la upimaji. Ni kweli tumekuwa na changamoto kubwa sana ya watu kubainishwa na ugonjwa wa Typhoid na UTI. Nimesema sana na ninaomba nitumie fursa hii kuongea na Bunge lako. Ukienda hospitali na ndani ya dakika tano Daktari akwambia UTI ama una Typhoid, naomba umwulize maswali ya msingi sana huyo daktari. Amejuaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaalam wetu sisi madaktari inahitaji kati ya masaa 48 mpaka 72 na achukue kipimo cha mkojo na achukue na kipimo cha damu kuja kukwambia wewe una ugonjwa wa Typhoid au una UTI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba sana na Waheshimiwa Wabunge mtusaidie kutoa elimu kwa jamii kuwahoji wataalam wetu wa afya kwa sababu wengi sasa wameamua kwa kutumia homa ya UTI na Typhoid kama chanzo cha kupata fedha, lakini kimsingi hatuna tatizo kubwa sana la UTI na Malaria kama inavyosemwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kumaliza hizi hoja kama nyingi zilivyokuwa zimejitokea na nitoe fursa sasa kwa Mheshimiwa Waziri aweze kuendelea na hoja nyingine. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kuwashukuru Wabunge wote pamoja na Kamati kwa maoni mazuri. Nami niwahakikishieni ma-crown yote tumeyachukua na tutayazingatia katika utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana wachangiaji wote; tumepokea michango 28 ya Wabunge ambao waliichangia hapa ndani Bungeni, 40 michango kupitia kwenye kamati lakini tumepata michango nane kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba Wizara yetu sisi ni Wizara mtambuka. Ni Wizara wezeshi na Wizara ambayo inasaidia sekta nyingine zote na kuwezesha sekta nyingine zote. Kwa nini kumeanzishwa Wizara hii, nataka nitumie fursa hii kutoa elimu kidogo kwa Wabunge, kwamba Wizara hii imeanzishwa mahsusi kuangalia jinsi gani sisi kama nchi wakati dunia inaongelea mapinduzi ya nne ya viwanda forth industry revolution ambayo msingi wake mkubwa ni TEHAMA, basi na sisi kama nchi tuweze kujiandaa katika msingi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inaongelea masuala ya digital economy na ukiangalia sasa hivi, ukiangazia miaka 10 iliyopita, makampuni makubwa duniani yalikuwa katika manufacturing, lakini sasa hivi ukiangalia makampuni makubwa yapo katika sekta ya TEHAMA. Kwa hiyo, sisi kama nchi ni lazima tuangalie na tuangazie huko.


Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kujibu swali ambalo ameniuliza Mheshimiwa Neema Lugangila ni kwamba ndiyo tupo katika maandalizi ya sasa hivi ya kuandika digital economy blue prints ya Tanzania. Kazi hiyo tumeshaanza hatua za awali na tunatarajia andiko hilo litaweza kuanza hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunataka kuangazia e-commerce na Wabunge wamesema, element za e-commerce tumeanza nazo nchini. Sasa hivi ukiangalia wafanyabiashara wanjanja ama vijana hawatumii sasa na wala hawaendi pale Kariakoo kukodisha fremu, mtu anaagiza mzigo wake anaweka nyumbani, anapiga picha anaweka kwenye mitandao ya jamii. Wewe ukitamani, unaingia katika mtandao ya jamii, unachagua pale, mnalipana kwa miamala ya simu, anamtuma boda boda anakuletea nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale hamna kodi ya jengo, hakuna leseni za TRA, wala leseni za biashara ni lazima na sisi tuwezeshe ili kuweka mifumo mizuri kuhakikisha kwamba e- commerce hata wewe sasa hivi unaweza ukaagiza mzigo nchi yoyote ya nje na mzigo wako ukaweza kukufikia. Huo utaratibu ambao tunakwenda nao wa anuani za makazi na postikodi, tunataka mzigo ukufikie wewe nyumbani pale pale ulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunaangazia sasa hivi kuhakikisha kwamba Serikali inamfuata mwananchi mkononi badala ya mwananchi kwenda kupanga foleni katika Ofisi za Serikali, tunataka ku-digitize service za Serikali ili mwananchi aweze kupata kiganjani, kodi
za ardhi, masuala haya ya umeme na huduma nyingine za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaangazia vilevile kuhakikisha kwamba huduma za jamii, hawa Walimu wachache tuliokuwa nao nchini hao hao tuweze kuwatumia waweze kutoa huduma za elimu katika maeneo mengine ambayo wana-shortage ya Walimu. Tuangazie kwamba badala ya Waziri wa Elimu kuhangaika kuchapisha vitabu, tunaweza tukatengeneza DG e-books na kuweza kuzisambaza na mwanafunzi akawa na kitabu chake kwa njia ya mtandao. Tukaachana na hizi library ambazo zimejazana vitabu vikuu vikuu, hizo space zikageuzwa kuwa madarasa badala yake mtoto akawa anasoma na akapata kitabu pale pale alipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaangazia kwamba Madaktari wetu wachache tuliokuwa nao waweze kutoa huduma kwa maeneo mengine ya pembezoni ambapo hakuna Madaktari Bingwa. Hilo tumelianza katika upande wa teleradiology ambapo sasa hivi tunafanya installation ya digital x-ray, Madaktari wetu Bingwa ambao wanaweza wakasoma x-ray, MRI na vitu vingine, picha inaweza ikapigwa Tandahimba ikatumwa Dar es Salaam pale MOI ikasomwa na majibu ndani ya dakika 15 yakarudishiwa kule kule alipo mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kuangazia katika Sekta ya Kilimo, mkulima kule kule alipo akiwa na simu janja aweze kupata ushauri kuhusiana na masuala ya mbegu, masuala ya wadudu waharibifu, kuhusiana na mbolea na kuhusiana na masoko kule kule katika eneo ambalo yeye yupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kuangazia mchango wa sekta hii katika uchumi na pato la Taifa letu. Watalaam wanasema tukiwekeza katika Sekta ya TEHAMA by 10 percent inaweza kusaidia kukuza Pato la Taifa kwa zaidi ya asilimia 1.5. Sasa nini tunachotaka kukiangazia, katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi imetuelekeza sisi, kuhakikisha kwamba tunakuza Mkongo wa Taifa kutoka asilimia 45 tuliokuwepo sasa hivi hadi kufikia asilimia 80 na kuongeza mahitaji ya matumizi ya internet kutoka asilimia 43 mpaka asilimia 80 ambayo imeelezwa pale katika Ilani ya Uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua gani ambazo tunazichukua sasa hivi? Mheshimiwa Naibu Waziri ametoka kusema, sasa hivi tunavyoongea Mkongo wa Taifa tunakwenda kufikia kilometa 8,319. Katika mwaka huu wa fedha bajeti kama Wabunge watatupitishia tena hapa tutakwenda kujenga kilometa 1,880, tumeshafika katika Makao Makuu yote ya Mikoa, bajeti wakitupitishia Wabunge tunakwenda kufikisha katika Makao Makuu ya Wilaya zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo letu tukifika 2025 tunataka tufikie Mkongo kilometa 15,000. Sasa hivi tumeweza kufikia nchi zote za Jirani, sasa hivi tunafanya upembuzi yakinifu tuweze kuunganisha na DRC. Changamoto ambayo tumeipata sasa hivi kwa sababu ya kina cha Ziwa la Tanganyika ndiyo tunajaribu kuangalia teknolojia gani ambayo tunaweza kutumia ili kuhakikisha kwamba mkongo na sisi tunaweza tukaufikisha kule DRC. Lengo letu na sisi tuwe ni hub ya TEHAMA katika Afrika Mashariki na tuweze kuwafikia wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea na nikimaliza Bunge naenda Mtambaswala sasa hivi tunafanya kwenye connectivity na Msumbiji, ili kuhakikisha kwamba mawasiliano yetu na sisi tunawafikishia kule Msumbiji. Sasa na hatua gani nyingine ambazo tunaendelea kuzichukua ili sasa tuweze kuwa na usimamizi mkongo ambao ndiyo highway, ndiyo njia kuu ya mawasiliano na ndiyo moja ya njia kuu ya uchumi kama ilivyo reli, barabara pamoja na bandari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkongo wa Taifa nao ni moja ya njia kuu, tutakapokuwa tunaongelea huko masuala ya barabara na tukumbuke vile vile suala la Mkongo wa Taifa ambao ndiyo njia kuu ya mawasiliano ndani ya nchi yetu. Mawasiliano sasa hivi si anasa ni haki ya msingi ya kila Mtanzania. Tunakwenda kuboresha usimamizi wa mkongo na tunakwenda kuanzisha chombo ambacho kazi yake kikiamka asubuhi ni kusimamia, kuendesha na kuendeleza suala hili la mkongo, tumeshaanza mchakato huo na tunaamini ifikikapo Julai Mosi, jambo hili tutakwenda kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo suala la kuwekeza katika miundombinu halitoshi peke yake, tunataka sasa tuwekeze katika digital literacy. Tukiangalia Watanzania wengi bado hawana uelewa mzuri wa matumizi ya internet, hata sisi Wabunge tunatumia chini ya asilimia 50 ya uwezo wa simu zetu. Tunakata tu-invest kuhakikisha kwamba tunajenga digital literacy, elimu ya kutosha katika masuala ya haya ya TEHAMA, lakini sambamba na hilo kuhakikisha kwamba tunakuwa na matumizi sahihi na mazuri ya internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya hayatakuwa na tija kama uwezo wa Watanzania kuweza kumudu kununua simu janja na vifaa mpakato. Sasa hivi tunataka kujielekeza kuhakikisha kwamba vifaa mpakato vinapatikana kwa gharama nafuu. Moja ya mkakati ambao tunao ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na viwanda vya ku-assemble ama kujenga viwanda ambavyo vitatengeneza simu janja hapa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunataka kuongeza wigo wa internet na tumewasikia Waheshimiwa Wabunge, ni kweli mwanzoni tulipokuwa tunaanza mikakati yetu ilikuwa lengo ni kuwafikishia mawasiliano na ndiyo maana mitandao yetu mingi ilikuwa 2G, lakini tumekubaliana sasa minara yote tunayoenda kujenga sasa hivi itakuwa ni 3G kwenda juu, ili kuwezesha sasa Watanzania walio wengi waweze kupata huduma za internet. Hakuna mtu ambaye anayesema kwamba vijijini eti nao hawahitaji internets, tunataka hata wale wa vijijini waweze kutumia internet kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kujiletea maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda ku-harmonize system, sasa hivi kama unavyofahamu miaka mitano iliyopita mifumo yote nchini ilikuwa ya kutoka nje ya nchi, lakini sasa hivi tumepiga hatua mifumo mingi ya TEHAMA ndani ya nchi sasa hivi asilimia 80 tunaitengeneza hapa hapa nchini. Changamoto ni kama hizi ambazo zimejitokeza kwa hii katika mifumo ya LUKU, bado kuna changamoto ya mifumo kuingiliana, bado kuweka mifumo ya backup na bado kuna mianya kidogo ambayo inaweza ikawa ni hatarishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote Wizara yetu itaendelea kuyasimamia na kuhakikisha kwamba tunaweka mifumo mizuri na sahihi. Pia tutahakikisha kwamba hii mifumo ambayo imetengenezwa na vijana wetu wazalendo inakuwa ni robust na inaweza ikasimama na tunakuwa na mifumo mingine ya backup ambayo inaweza ikasaidia, pakitokea tatizo basi kunakuwa na njia mbadala ya kuweza kupata huduma zile husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunakwenda kufanya maboresho ya sheria. Wizara yangu na sekta yangu ni sekta ambayo inakwenda kwa kasi sana. Tumekuwa na sheria ambazo zimekuwa ni za muda mrefu sana. Niombe kusema na nasimama mbele ya Bunge hili kusema, sitaki kukumbukwa kama Waziri ambaye alikuwa ni Polisi wa sekta, nataka nikumbukwe kwamba ni Waziri ambaye alikwenda kuleta mapinduzi makubwa katika Sekta ya TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie, sitaki kukumbukwa kwamba Waziri ambaye alienda kuminya na kuwa Polisi wa sekta, nataka nikumbukwe kwamba ni Waziri aliyeweza kuweka mazingira wezeshi ya Sekta ya TEHAMA kukua ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Wizara tunakwenda kufanya mabadiliko makubwa sana ya kimuundo ya taasisi zangu, lakini muundo wa kisheria, ikiwa ni pamoja na hawa vijana wetu ambao wanajiajiri kupitia TEHAMA. Kijana ni MC anafanya shughuli zake za harusi, anarusha picha zake kwenye You Tube ili watu wengine mumwone umahiri wake wa kazi halafu sisi tunataka kumtoza kodi, hili tunataka tuondokane nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wetu hawa wasanii, wanatengeneza nyimbo zao, sasa hivi hawauzi cassette wala hawauzi flash, wanaziweka huko kwenye mitandao na huko ndipo wanapata mapato yao sisi tunaenda kuwaminya tena kule. Tunataka kwenda kufanya maboresho makubwa ambayo yatatengeneza mazingira wezeshi kuhakikisha hizi platform sisi tusiwe ni kizuizi bali tuwe ni watu ambao wanakwenda kuhakikisha kwamba hawa vijana wanaweza kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tutakwenda kuliangalia suala la visimbuzi nalo nimeshatoa maelekezo tarehe 21 watoa huduma, watoa huduma sijui wa visimbuzi wote, watu wa television wote tarehe 21 nimewaambia wakae, wakae kama wadau wakubaliane yale makubaliano sisi Serikali tutayachukua na tutayabariki, tunataka tufanye mapinduzi makubwa hata katika hii tasnia ya wenzetu ya television.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunahitaji tuwe na mabadiliko ya fikra na sisi kama Wabunge tunahitaji tufikiri upya sasa hivi katika sekta hii TEHAMA, Tanzania tupo nyuma sana, wenzetu Kenya, Rwanda, Ghana, Nigeria wapo mbali, kuna vitu vinaitwa startup sasa hivi. Vijana wa sasa hivi hawatengenezi makampuni ya wajukuu wao kuja kurithi, wanatengeneza makampuni ambayo lile wazo lake likikubalika likaingia katika soko anauza, anaenda kuanzisha kampuni mpya. Wale vijana hawana hela wana mawazo na wazo lake lile ndiyo hela. Ni lazima tuwatengenezee mazingira wezeshi hawa vijana yao ili kazi ziweze kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vijana wa software development, nawafahamu wanafanya kazi kubwa Israel, wanafanyia kazi Uingereza, ni Watanzania, lakini sisi hatuwatambui na wala hatuwatumii. Nimeongea na vijana baada ya Bunge hili, naenda kukutana na Tanzania Startup
Association, kukaa na kuangalia mahitaji yao na pale tutakapohitaji tutawaleta Waheshimiwa Wabunge mabadiliko ya sheria ili kutengeneza mazingira wezeshi kwa hawa Startups. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimenong’ona na Waziri mwenzangu wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, wasanii Mheshimiwa Mwinjuma tumewasikia tutakuja tukae tuongee na nyinyi tuangalie challenge zenu, tuangalie hayo masuala ya aggregation na tuangalie jinsi gani tunaweza kufanya ili sasa tupige hatua kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la TTCL, ni kampuni yetu na katika Ilani ya uchaguzi imeelezwa kwamba, tunahitaji tuiboreshe kimenejimenti na kiuwezeshaji ili iwe ni kampuni yetu ya kimikakati, ni lazima na sisi kama Serikali tuwe na kampuni yetu ya kimkakati ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili sisi kama Wizara na tukumbuke kwamba Waheshimiwa Wabunge sasa hivi sisi Wizara yetu ina miezi mitano tu, lakini hili na sisi tumelichukulia kwa uzito ambao unastahili. Tumeshakaa na wenzetu wa TTCL wameandika andiko lao la mahitaji yao na tumeshalipokea na tumeshalipitia na tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Fedha, ili kuangalia huo mkakati wa kibiashara ambao wanataka kuja nao jinsi gani sisi kama Serikali tutakwenda kuwa-support. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeanza kufanya mapitio ya sheria ili kuhakikisha sasa na hili shirika letu ambalo linajiendesha kibiashara kuna sheria nyingi ambazo zinatukwaza. Kwa hiyo, mambo hayo mengine kwa mfano shirika letu sasa hivi haliruhusiwi kununua minara ambayo imetumika. Kwa hiyo, nayo tunataka kwenda kufanya mabadiliko ya sheria za manunuzi, ili tuwaruhusu kuweza kufanya manunuzi ya minara ambayo imetumika ama vitu vingine na kurahisisha utoaji huduma zao kama wanavyoweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme kwamba tu kuna maboresho makubwa sana tunakwenda kuyafanya katika nyanja hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie suala la digital taxes na hili nilishawahi kulisema lakini nadhani ilitafsiriwa vibaya, lengo letu sio sisi kuja kuweka kodi kwenye Whatsaps, Instagram na twitter huko siko. Lengo letu wale wakubwa sisi tunatumia mitandao hii bure, wanaotengeneza ni wale wakubwa ambao wanapata fedha nyingi za matangazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo letu ni sisi tuwafikie wale sio mlaji huyu wa mwisho ambaye anakuja anatumia Instagram, Twitter na Facebook. Kwa hiyo, sisi tunajiangalia jinsi gani ya ku-analyze potential ya digital taxes kule badala ya kumbana mtumiaji huyu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili nilitaka nalo niliseme, lakini sambamba na hilo tunakwenda kufanya maboresho ya sheria ya kulinda faragha za watu. Tuna data nyingi tunazi-generates unapotumia mitandao hii hii unapokwenda sehemu mbalimbali, kuna taarifa nyingi sana za kwako ziko pale zinaeleaelea. Kwa hiyo, tunakwenda kutengeneza sheria mpya ya data privacy na data protection lengo sio kuminya uhuru wa watu, lengo ni kukulinda wewe taarifa zako ambazo zinauzwa huko duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo tutakwenda kuwekeza katika innovation hub natamani kuona miaka mitano ijayo Tanzania na sisi tunakuwa seal convert vijana wabunifu, sectoral developers, masuala ya cyber security, internet of things, block chain technology, artificial intelligence, tunajenga capacity ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema tunatambua jambo hili la uhalifu wa mitandao na usajili wa online tunakwenda kuboresha mifumo na hiyo tarehe 26, tutakaa na Mawaziri wenzangu tuangalie njia bora zaidi ya kuangalia jinsi gani tunaweza kubana katika usajili huu wa line za simu. Ikiwa ni pamoja tunaweza tukaja na zoezi tena jipya la uhakiki wa watu wote ambao wamejisajili kwa njia ya biometric, ili kuhakikisha kwamba ni watu ambao wana kadi za simu wote wamesajiliwa na tunaweza kuweka mifumo ya kuweza kuwabaini. Na teknolojia tunayo ya kuangalia jinsi gani na kuweza kuzi-block hizo simu ambazo zinaweza kuwa zinatumika kwa njia ya kiuhalifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimejielekeza zaidi katika kutoa elimu zaidi kuliko kuwaadhibu kwasababu, nimeona kwamba watu wengi hatujui sheria, watu wengi hatujui haki zetu, watu wengi hatujui matumizi sahihi ya mitandao. Kwa hiyo, na mimi nataka kama Waziri kujielekeza katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu mizuri niwahakikishieni yote haya ambayo mnayasema tunaenda kuyafanyia kazi na kuweka mipango mikakati ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na Tanzania ya TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia katika Azimio hili, kuhusiana na Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Madawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba huu umekuja umechelewa lakini ni mkataba ambao ni muhimu sana. Kama walivyotangulia kusema wenzangu michezo ni afya, michezo ni ajira, michezo ni mahusiano na michezo inajenga undugu na amani. Katika dhana hii ya michezo kumekuwa na tatizo kubwa tena kubwa sana kuhusiana na baadhi ya washindani kutaka kupata ubora ama ushindi katika njia za mkato.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi katika dunia ambao wanafuatilia vyombo vya habari watakuwa wanajua wanariadha wa Kenya ambao wamekuwa wanasifika sana duniani wamepata kashfa ya matumizi ya madawa ya kulevya. Vilevile kwa upande wa Urusi maabara ambazo zimekuwa zinapima matumizi ya madawa ya kulevya nazo zimeingia matatani. Mara nyingi nchi ambazo zinapata matatizo haya huwa zinakosa sifa na zile ambazo zimekuwa zimejengeka kwa muda mrefu kuhusiana na washindani wao na inatia mashaka kuhusiana na wanariadha wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Daktari athari za madawa ya kulevya ni kubwa sana, wachangiaji waliopita wamezisema, siyo tu kwa kipindi kile ambapo wanariadha wanashiriki katika michezo lakini hata baada ya miaka kumi, ishirini, thelathini baada ya kuacha kutumia madawa haya watu bado wana athari za kimwili, kisaikolojia na kiakili. Kwa hiyo, mkataba huu umechelewa na naunga mkono tuuridhie na nitawaomba Waheshimiwa Wabunge wote na sisi tuukubali kwa sababu una manufaa makubwa sana katika suala zima la michezo katika nchi yetu. Hata hivyo, wakati tunaelekea kuuridhia mkataba huu nitaomba tu vile vile tuangalie katika mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, moja; tuhakikishe kwamba tunatoa elimu ya kutosha kuhusiana na hivi vitu ambavyo ama madawa ama zile njia ambazo zimedhibitiwa katika mkataba huu; sio kila mwanamichezo anaelewa hili na siyo mamlaka zote zinaelewa hili. Kwa hiyo, tujikite zaidi kupitia Wizara husika kuhakikisha kwamba tunajenga, tunatoa elimu ya kutosha kwa wanamichezo vilevile katika mamlaka mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili; tujenge uwezo wetu wa ndani wa kuweza kubaini matumizi ya madawa haya; maana yake ni kwamba sasa tuwe na maabara zetu, zitasajiliwa na ambazo zitakuwa zinatumika katika mashindano yetu ya ndani tuwe na uwezo wa kuweza kubaini baadhi ya matumizi haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo naliomba ni kutoa elimu vilevile kwa Madaktari wa michezo. Inawezekana mtu akapewa dawa pasipo kujua dawa hii inakuwa na athari ama inaweza kuwa ni stimulants ama ikawa na madhara ama ikawa ni sehemu ya yale madawa yasiyoruhusiwa na mtu ameitoa tu. Kuna madawa kwa mfano, kuna dawa zingine tu za mafua ambazo mtu akipewa zinakatazwa kwa mujibu wa mkataba huo. Kwa hiyo, nataka tutoe hii elimu kwa Madaktari wa michezo, lakini sasa tuwe na mtatibu wa kusajili Madaktari wa michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nami naunga mkono hoja hii ya kuridhia Mkataba huu, umechelewa kuja, lakini ni Mkataba muhimu sana katika ushiriki wa Tanzania katika masuala ya michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia katika maeneo mawili ambayo yaligusiwa na wachangiaji katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni mabadiliko ya kisheria, kuna sheria mbili ambazo tunatarajia kuzileta Bungeni kwa mara ya kwanza. Tunatambua kumekuwa na changamoto katika ugharamiaji wa matibabu na hivyo kama Serikali tunakusudia kuleta Muswada wa Bima ya Afya kwa wananchi wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, tunatambua vilevile katika kufikia malengo ya 90-90-90 kwa maana ya asilimia 90 ya watu wote ambao wanaishi na Virusi vya UKIMWI tuweze kuwafikia na kuwapima, asilimia 90 ya wale ambao wamepimwa waweze kupata matibabu na asilimia 90 ya wale ambao watapata matibabu tuweze kufubaza kabisa Virusi vya UKIMWI, tumeona kwamba kumekuwa na changamoto hususani katika kundi la vijana na wanaume, hivyo tunataka kuja na mabadiliko ya sheria ili kuruhusu upimaji binafsi lakini vilevile kushusha umri wa upimaji kufikia miaka 15. Taratibu zote za mabadiliko haya ya sheria yako katika ngazi mbalimbali ndani ya Serikali na pindi taratibu hizi zitakapokamilika Miswada hii italetwa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo liligusiwa na wachangiaji ni kuhusiana na hali ya magonjwa nchini. Kwa muda mrefu tumekuwa tunapambana na magonjwa ya kuambukiza lakini sasa hivi tumeanza kuona ongezeko kubwa sana la magonjwa yasiyoambukizwa kwa maana ya kisukari, pressure, kiharusi na magonjwa ya figo. Sisi kama Serikali tumeona tunahitaji tuanze kujipanga upya, hivyo tunataka tuangalie mtiririko mzima wa huduma za afya kama alivyokuwa ameongelea Mheshimiwa Mukasa kuangalia masuala ya elimu, kinga, tiba na huduma ya utengamao. Awali tulikuwa tumejikita sana katika masuala ya tiba tukaacha haya maeneo mengine. Ili sasa tuweze kupambana vizuri na magonjwa yasiyoambukiza tunahitaji tuhakikishe kwamba huu mtiririko mzima tunauzingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Afya tuko katika hatua za mwisho kuanzisha Mpango wa Taifa wa Magonjwa Yasiyoambukiza kama ilivyo kwa magonjwa ya UKIMWI, TB na Malaria. Tunataka tuje na Mpango wa Magonjwa Yasiyoambukiza ili tuweze kuwa na utaratibu mzuri wa kudhibiti magonjwa haya. Tutaweka utaratibu ambao utaanzia katika ngazi ya Taifa mpaka ngazi za kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia, na kama itakupendeza ntaomba dakika zangu mbili nimpatie Mheshimiwa Zitto Kabwe aweze kuendelea nazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa uwasilishaji wa taarifa nzuri ambayo imesheheni mambo makubwa ya msingi. Nitajielekeza moja kwa moja katika suala la Mji mpya wa Kigamboni. Katika ukurasa wa sita wa taarifa hii Kamati hii ya Bunge ilitembelea Wakala wa Uendelezaji wa Mji Mpya wa Kigamboni na naomba ninukuu walichokisema:-
“Kamati ilifanya ziara katika Ofisi ya Wakala wa Uendelezaji wa Mji Mpya wa Kigamboni tarehe 18 Machi, 2016 na kupokea taarifa kuhusu maendeleo ya mradi. Kamati haikuridhishwa na hatua ya Serikali katika utekelezaji wa mradi huu na hadi wakati Kamati inapokea taarifa za utekelezaji wa miradi hakukuwa na fedha zozote zilizotengwa kwa ajili ya uendelezaji wa mradi ikiwa ni pamoja na kulipa fidia katika maeneo yatakayojengwa miundombinu.
Kutokana na hali hii hakukuwa na mradi wowote ulioonekana kuanzishwa na hivyo kupoteza maana halisi ya kuwa na mradi na uanzishwaji wa Wakala. Hali hii imesababisha Serikali kupoteza fedha za kulipia pango za wakala na kuwa na watendaji ambao hawana majukumu ya kutekeleza. Kamati inashauri Serikali iachane na mradi huu kwa kuwa umechukua muda mrefu bila kuwa na utekelezaji wowote.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naunga mkono hoja hii, ni mwaka wa tisa tangu Serikali itoe azimio la kujenga Mji wa Kigamboni. Hadi hivi sasa wananchi wa Kigamboni hawawezi wakajenga wala wakauza ardhi yao wala kuiendeleza, inawaletea umaskini mkubwa sana. Nami naunga mkono ripoti ya Kamati. Katika mwaka wa jana wa fedha Serikali haikutoa hata senti tano na wala hivi tunavyoongea hakuna hata senti tano ya fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa jana niliitisha mikutano ya wadau wa Kigamboni, Wenyeviti wangu wote wa Serikali za Mtaa, Madiwani na Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Temeke kabla halijavunjwa na tukatoka na azimio kwamba moja, KDA ivunjwe na mamlaka yake yakabidhiwe katika Halmashauri mpya ya Kigamboni.
Pili, suala zima la uendelezaji wa Kigamboni sasa kwa kuwa Kigamboni sasa hivi ni wilaya inayojitegemea, ni halmashauri inayojitegemea, ina Idara ya Mipango Miji ambayo ina sifa na vigezo vya kusimamia uendelezaji wa Kigamboni; muda wa miaka tisa umetosha sasa tunaomba sisi kama Wanakigamboni tuivunje KDA na shughuli zote zikabidhiwe katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaliomba sasa Waheshimiwa Wabunge hili nalo, pamoja na kwamba mmelitoa kwenye preamble, naomba liingie kama azimio ili sasa Serikali itoe msukumo zaidi, pamoja na mapendekezo ambayo tumeyaleta sisi kama Wanakigamboni hili sasa liwe ni azimio la Bunge ili sasa baada ya hapo Serikali iweze kutekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina mengi ya kusema, naomba niishie hapo. Nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa ya kwanza ya kuwa mchangiaji katika hotuba ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Nianze kwa kumpongeza sana Waziri Mheshimiwa William Lukuvi, Naibu Waziri Mheshimiwa Angeline Mabula, Katibu Mkuu Dkt. Kayandabila na safu yake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kuifanya katika Wizara ya Ardhi. Kwa mara ya kwanza nitaanza kuiongelea vizuri Wizara ya Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mitano ambayo nimekuwa Mbunge katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sijawahi kuunga mkono bajeti ya Wizara ya Ardhi, inawezekana leo ikawa ndiyo mara yangu ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la kwanza ambalo nilitaka niligusie ni suala la premium. Mheshimiwa Waziri ameongea katika hotuba yake kwamba amepunguza premium kutoka 7.5 percent kwenda asilimia 2.5. Tunatoa pongezi nyingi sana kwa Serikali, lakini bado tunaamini kwamba kiwango hiki bado ni kikubwa sana. Waende wakaliangalie tena. Katika suala la mashamba makubwa ambayo wamekuwa wanayahimiza wananchi wayapime, kikwazo kimoja cha kupanga Miji na upimaji imekuwa ni premium. Kwa hiyo, naomba waende wakaiangalie upya ili kama ikiwezekana tuipunguze zaidi na itatoa hamasa kwa wananchi kupima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni viwango vya land rents; kodi za ardhi nazo bado kuna wakati walipandisha, nadhani sasa wamefanya marekebisho. Suala hapa siyo kupandisha viwango, suala hapa ni kuhamasisha wananchi waweze kuwa wanalipia. Tukiongeza viwango vikawa vikubwa sana, ulipaji nao utakuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nataka sana Wizara nayo itusaidie, asilimia 30 ya mapato yale ya land rent yanayotakiwa kurudishwa katika Halmashauri, mpaka wakati tunatengana na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke tulikuwa tunaidai Wizara ya Ardhi takribani Sh.3,000,000,000/=. Ni fedha nyingi sana ambazo zingeweza kutusaidia katika maendeleo ya Halmashauri zetu. Sasa nadhani ifike mahali kama inashindikana fedha ile kwenda na wao wakaturejeshea 30 percent, kwa nini sasa tusipitishe sheria tufanye mabadiliko tu-retain ile 30 percent na sisi tuwapatieni ile hela nyingine iliyobaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo nataka kuligusia ni master plan ya Mkoa wa Dar es Salaam. Dar es Salaam inakuwa kwa kasi kubwa sana, lakini utengenezaji wa master plan umekuwa unakwenda muda mrefu sana. Nimeona katika ripoti yao wanaongelea mwezi Agosti, naamini Agosti itakuja nayo itakwisha. Tungependa kuona ifikapo mwisho wa mwaka huu tuwe na master plan ya Dar es Salaam, ujenzi holela unatapakaa kwa kasi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne ambalo ninataka kuligusia ni mradi wa viwanja 20,000 katika Jimbo langu la Kigamboni, hususan katika eneo la Kibada. Wananchi walionunua viwanja vile, walilipa premium ambayo inaendana na utengenezaji wa miundombinu. Mpaka sasa hivi tunavyoongea kuna wananchi wa Kibada wanaelea, kuna viwanja wamewapa kwenye mabonde, sasa hivi kuna wananchi wa Kibada wanashindwa kufika majumbani kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kibada hawana miundombinu ya kufika katika makazi yao na nitamwomba sana Mheshimiwa Waziri baada ya bajeti yake twende Kibada akawaone wananchi wale ambao walilipa fedha na wanalipa kodi ya ardhi, wanaishi kwa shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ambalo nataka kuliongelea ni suala la Kigamboni. Serikali ilikuja na mpango wa Kigamboni mwaka 2008 tunavyoongelea sasa hivi ni mwaka wa tisa, wananchi wale hawajengi, hawakarabati, hawauzi wala hawakopesheki. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri tangu ameingia katika Wizara ile, tumeweza kufanya kazi kubwa sana mimi na yeye na namshukuru sana chini ya uongozi wake, yale ambayo wananchi wa Kigamboni tuliyokuwa tumesimamia, ameweza kuyasimamia na kuyatekeleza kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana yeye na safu nzima ya Wizara yake. Hatua tuliyofikia ni nzuri sana na ndiyo maana mnaona Mbunge wa Kigamboni sasa hivi ametulia, la sivyo siku za nyuma hapa pangekuwa hapatoshi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna lile ombi ambalo tumeleta kwenu Serikalini na ambalo nashukuru Mheshimiwa Waziri ameligusia kwa kidogo. Kuwepo mamlaka mbili za kupanga mji inaleta kero na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuvunja CDA. Sisi pia sasa
tunasema KDA hatuitaki. Tunaomba mradi ule uletwe chini ya Halmashauri mpya, chini ya uongozi mpya wa Kigamboni ili sisi wenyewe tukausimamie. Mheshimiwa Waziri akiweza kulitekeleza hilo, tutakuwa marafiki wa kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, machache nakushukuru sana na kwa mara ya kwanza naunga mkono bajeti ya Wizara ya Ardhi. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na niwapongeze sana watoa hoja wote wamewasilisha vizuri sana na mimi nilitaka nichangie katika hotuba ambayo, imewasilishwa na Kamati ya Bajeti na hususani nataka nijielekeze katika kipengele ambacho aligusia daraja la Tanzanite.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wakazi wa Kigamboni tuna daraja linaitwa daraja la Nyerere ama kwa jina limezoeleka kama daraja la Kigamboni. Daraja hili limeanza kutumika tangu mwaka 2015 na limekuwa ni daraja pekee ndani ya nchi yetu ambalo linatozwa tozo kwa mwananchi kuvuka. Wananchi wa Kigamboni hawana mbadala ili mwananchi wa Kigamboni afike mjini aidha apite Ferry ambako anapanda pantoni, analipa tozo au inabidi apite darajani kwa mguu ama kwa wale ambao wana magari na vyombo vya usafiri lazima alipe tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, daladala moja ambayo inavuka pale inachajiwa kati ya shilingi 5,000 kwa kila trip ambayo inavuka pale zikiwa trip 10 za kwenda na kurudi hiyo ni shilingi 100,000. Kwa hiyo, wananchi wa Kigamboni wanakosa usafiri wa njia route ndefu ambazo wananchi wakazi wa maeneo mengine wanazipata. Mwananchi wa Kigamboni ili afike mjini anahitaji nauli tatu mpaka nne tofauti na wakazi wengine wa Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wananchi wa Kigamboni wamenituma kuulizia wamesikia kauli ya Serikali kwamba daraja la Tanzanite litakuwa bure, wakati wakazi wa Kigamboni wao ambao wanajiita ni masikini wanatozwa tozo ili waweze kuvuka kwenda mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawana mbadala kama walivyo wakazi wengine wa Oysterbay na Masaki ambao, wana barabara ya Salender sisi ukipita kwenye Kivuko na ukipita darajani ni lazima ulipie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Kigamboni wameniomba niwaulizie kwa niaba yao je, ni kwa nini tu peke yao ambao ni daraja pekee, ambao wanapaswa kulipia na wakati wananchi wa Kigamboni wanachangia katika ujenzi wa madaraja mengine. Hata kama hili daraja limejengwa kwa mkopo wa Wakorea na ninatambua kwamba daraja lile la Kigamboni limejengwa kwa mkopo kutoka NSSF. Kwa nini Serikali isilibebe kama inavyobeba mikopo ya madaraja mengine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali ilichukulie suala hili kwa uzito unaostahili wananchi gharama za maisha/ wananchi wa Kigamboni ni, kubwa sana na wananchi wa Kigamboni hawana mbadala wa kwenda mjini zaidi ya kupitia kwenye Kivuko na kutumia daraja. Tofauti na wakazi wengine wa Masaki, Oysterbay ambao wana barabara mbadala ya kuweza kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe kwamba Serikali itafakari kuondoa tozo katika daraja lile la Kigamboni Serikali ibebe mzigo wa deni lile la NSSF, ili na wananchi wa Kigamboni nao wapate nafuu ya gharama za maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kupata nafasi ya kuweza kuchangia katika mpango, lengo langu si kuyarudia yale ambayo yametoka kusemwa na wenzangu lakini mengi yameshagusiwa kuhusiana na maeneo ya kimkakati ambayo Bunge linashauri Serikali iende kuyaangalia ambayo yatasaidia kukuza uchumi wetu sambamba na hilo litakwenda kuzalisha ajira mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mfumuko wa bei nalo limegusiwa ni jambo ambalo linawaathiri wananchi wengi, ukizingatia kwamba sasa hivi tuna tatizo la ukame bei ya vyakula itaenda kupanda mara dufu, mimi siyo mchumi lakini naiona hii hali ambayo tunakwenda nayo tusipoweka mikakati thabiti ni jambo ambalo litatuletea shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijielekeza nirudi tena katika mpango. Nimesikiliza sana michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi, kuna mambo ambayo na mimi nayaona kuna changamoto. Jambo la kwanza katika mipango hii ambayo tunaileta Bungeni kila mwaka, kunakosekana muunganiko mpango wa mwaka jana hakuna muunganiko na mpango wa mwaka huu na mpango ambao tunaumaliza sasa hivi hauna muunganiko na ule ambao tumepita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunaona kwamba hakuna mwendelezo. Vilevile jambo la tatu ambalo naliona ni kwamba tunatengeza mpango ambao siyo shirikishi na ukiangalia mikakati ya sekta mbalimbali ukija ukiangalia hapa katika mpango huu huwezi kuuona huo muunganiko. Kwa hiyo, inaonekana kwamba Wizara ya Fedha ipo kivyake, Wizara nyingine ambazo za kisekta nazo ziko kivyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nitoe ushauri na mchango wangu utakuwa mfupi sana. Jambo la kwanza ambalo naliona nataka kuishauri Serikali ni kuirudisha Tume ya Mipango. Wizara ya Fedha ibaki kuwa Wizara ya Fedha isimamie Sera ya Fedha, isimamie ukusanyaji wa fedha, isimamie matumizi ya fedha. Sasa hivi ukiingalia ile iliyokuwa Tume ya Mipango imemezwa ndani ya Wizara ya Fedha na Mipango na majukumu yake yamefinywafinywa sana huioni kujitokeza. Kwa hiyo, nashauri ile Tume ya Mipango irudi iwe chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Rais na kazi iwe sasa kufanya yale ambayo nimeyaainisha kwamba itusaidie kukaa na kuangalia mpango mzima wa maendeleo wa muda mfupi, wa muda wa kati na muda mrefu, kutengeneza mwelekeo, kutengeneza mwendelezo vilevile na kuainisha vipaumbele ambavyo sasa tutakuwa tunakaa tunaviongelea ambavyo vitakuwa na tija katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ushauri wangu wa pili. Tulianza lakini hapo katikati tukaivunja kitu kinaitwa Presidential Delivery Bureau ama Presidential Delivery Unity tunahitaji hiki chombo. Sababu ambazo nazisema kwa nini tunakihitaji hiki chombo ni kwa sababu hiki kitatusaidia katika masuala ya uratibu ambayo ni changamoto tunaiona. Kwa sababu ukiangalia sasa hivi kila sekta inaonekana kama ina-operate kivyake vyake, sasa tukiwa na chombo kama hiki, kitatusaidia katika hii miradi ya kimkakati kuwa na uratibu mzuri, itafanya tathmini na ufuatiliaji wa hii miradi mikubwa ambayo tunaitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauiri wangu wa mwisho. Hii inatuhusu sisi kama Wabunge, Kamati yetu ya Bajeti inafanya kazi nzuri sana, lakini inaitwa Kamati ya Bajeti. Mimi nilitaka tu na Mheshimiwa Spika yupo hapa ninaomba na kushauri tupanue wigo wa Kamati hii tuuite Kamati ya Fedha Mipango na Ufuatiliaji, ili hii sasa ikae kuangalia ule mtiriko mzima tangia tunaweka mipango, fedha gani tunazibajeti? zinakuwa disbursed kwa kiasi gani? Na hii ndiyo changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatengeneza bajeti hapa lakini fedha ambayo inaenda kutolewa mwisho wa siku hailingani na kile ambacho tulikuwa tumekibajeti. Sasa tukiwa na Kamati ya Bunge ambayo itakuwa inafanya ufuatiliaji pamoja na zile Kamati zetu za kisekta itatusaidia sana. Kwa hiyo mimi ushauri wangu ni kuwa, hii Kamati yetu ya Bunge ya Bajeti iwe ni Kamati ya Fedha, Mipango na Ufuatiliaji, tukienda kwa staili hii itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nimalizie kuhusu Dar-es-Salaam. Ukiangalia ina asilimia Nane ya wakazi wa Tanzania nzima, lakini uchimi wa Tanzania hii asilimia zaidi ya themanini unatoka Dar-es-Salaam. Sambamba na hilo ukiangalia wingi wa magari yako Dar- es-Salaam, ukiangalia miundombinu ya Dar-es-Salaam hailingani na uwekezaji uliopo pale. Vilevile ukiangalia Dar es Salaam tunafanya uwekezaji mkubwa wa reli ya SGR, tunafanya upanuzi wa Bandari hivyo unaendelea, tunaanza kufikiria vilevile kuwa na Bandari ya Bagamoyo, lakini ili uweze kufika Bagamoyo lazima upite Dar-es- Salaam ili uweze kufikia reli ya SGR lazima ufike Dar-es- salaam. Kwa hiyo, pamoja na hili Waziri Mwigulu Nchemba analijua, sisi kwetu wana Dar-es-Salaam wa DMDP ni mradi wa kimkakati na ni mradi muhimu sana kwa hiyo pamoja na zile barabara walizokuwa wanazisema lakini sisi kama Dar-es-Salaam tunazihitaji hizo barabara. Tunazihitaji hizo barabara jana, tulikuwa tunazihitaji leo na tunahitaji tufike kesho katika msingi wa kupata hizo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia taarifa ya Kamati mbili; Kamati ya Miundombinu na Kamati ya Maji na Kilimo.

Mheshimiwa Spika, mimi nitajielekeza katika Kamati ya Miundombinu na nimeipitia taarifa hii lakini nimebaini kwamba kuna eneo ambalo halijaguswa vizuri na hii inahusiana na Taasisi ya TEMESA. TEMESA ni taasisi ya Serikali inayosimamia masuala ya mechanical, electrical pamoja na masuala ya vivuko. Kwa kweli utendaji wa Taasisi hii ya TEMESA umekuwa siyo wa kuridhisha na huko tunapotoka kwenye Halmashauri zetu, magari yanayopelekwa TEMESA badala ya kwenda na kupona yanarudi yakiwa mabovu, gharama zinakuwa ni kubwa sana, TEMESA imekuwa ni dalali wa taasisi binafsi na gereji binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa leo nataka nijielekeze katika masuala ya menejimenti ya vivuko. Mimi ni Mbunge wa Jimbo ambalo ni lazima uvuke maji kwenda kufika katikati ya Jiji la Dar es Salaam. Katika hizi siku za karibuni kumekuwa na changamoto kubwa sana kwa wananchi wa Kigamboni kuhusiana na upatikanaji wa vivuko salama vyenye uhakika kwenda katikati ya Jiji la Dar es Salaam. Hivi karibuni tumepata kivuko ambacho kilikwenda kukarabatiwa cha MV-Kazi kimrudi lakini nacho kimerudi na changamoto kubwa sana pamoja na gharama ya bilioni 4.4 kukitengeneza kivuko kile.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tunategemea kupeleka panton kubwa MV-Magogoni Kenya, mimi kama Mtanzania nasikitika sana, tunao wazalendo ambao wanaweza wakavitengeneza hivi vivuko lakini kwa sababu ya taratibu tu za manunuzi tutakitoa kivuko chetu tutakipeleka Mombasa tutapeleka fedha za kigeni na tunakwenda kuua ajira, wakati huo huo tunasema tunataka tutengeneze ajira ndani ya nchi yetu. Hili mimi nilitamani sana Kamati ya Miundombinu ifanye mapitio ya mchakato wa manunuzi ya upatikanaji wa Mkandarasi wa utengenezaji wa MV-Magogoni.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani kampuni ya wazalendo ambayo imetengeneza boti zetu, inatengeneza meli zetu, tunasema kwamba haina uwezo wa kukarabati boti, hilo haliwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka nimalizie kutoa ushauri na nilitamani sasa hili nalo tuliongeze katika maazimio yetu kwamba TEMESA iangaliwe upya, kimfumo na kiutendaji. Nilitaka kushauri na kama Bunge lako nalo litatukubalia hususan katika upande wa vivuko. Pale kwangu Kigamboni wanavuka watu takriban watu 60,000 mpaka 80,000 kwa siku, yanavuka magari zaidi ya 2,000 lakini ni wazi kabisa usimamizi na uendeshaji wa vivuko vile umekuwa ni changamoto kubwa sana na iko siku tutapata maafa makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, imekuwa karibia kila wiki panton zinazimika baharini zinavutwa, mageti yanashindwa kufunguka yaani ni tafrani, haipiti wiki bila kupata malalamiko makubwa kuhusiana na vivuko vile. Sasa tusisubiri mpaka maafa yanatokea. Mimi nashauri kwa kuwa TEMESA wameshindwa kusimamia masuala haya ya vivuko ni vema vivuko hivi sasa vikapewa watu binafsi waweze kuvisimamia, kuviendesha na Serikali iweze kupata gawio kutokana na vivuko hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana kwamba katika moja ya Azimio la Bunge lako basi suala la TEMESA katika usimamizi wa vivuko liweze kuangaliwa na huduma hizo ziweze kupewa watu binafsi. Ninakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata na fursa ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Wizara hii kwangu kama Mbunge wa Jimbo la Kigamboni ni Wizara ambayo inagusa maisha ya kila siku ya wananchi wa Kigamboni. Kwa sababu hiyo nitajielekeza katika hoja tatu ambazo zinagusa Jimbo langu la Kigamboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni suala la Daraja la Nyerere. Daraja hili limejengwa kwa ubia kati ya Serikali na Shirika la NSSF. Daraja hili ni la kulipia; hoja ya wananchi wa Kigamboni bado iko palepale. Wananchi wa Kigamboni ni walipa kodi wa nchi hii. Wananchi wa Kigamboni michango yao na kodi zao zinachangia katika ujenzi wa madaraja mengine nchini lakini wananchi wa Kigamboni ni wananchi pekee katika nchi yetu ambao wao pekee wanachangia katika kuingia na kutoka Kigamboni. Kwa hiyo wananchi wa Kigamboni wamenituma kuja kusisitiza hoja yao ya kutaka daraja lile liondolewe ile tozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri, tulifanya mapunguzo ya tozo lakini bado wananchi wa Kigamboni wanasisitiza kwamba tozo ile iondolewe ili wapate ahueni ya maisha. Gharama za maisha kwa wananchi wa Kigamboni kwa kweli ni kubwa sana, hususan katika bidhaa zote zinazoingia Kigamboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nilikuwa nataka kuchangia ni suala la vivuko. Kivuko cha Kigamboni kinapitisha takribani watu 50,000 mpaka 60,000 kila siku na magari takribani 2,000 kila siku. Ni watu wengi sana. Lakini kumekuwa na changamoto nyingi sana katika kivuko kile. Kwanza, sehemu ya kusubiria abiria ni ndogo sana, hususan katika kipindi cha asubuhi na jioni. Lakini mifumo ya ulipaji fedha, kwa maana ya N-card nayo imekuwa na changamoto ya mifumo kuwa down, jambo ambalo linapelekea wananchi kupata usumbufu muda mrefu. Vile vile njia za kuingilia na kutokea katika kivuko hususani kwa upande wa Kigamboni na upande wa Magogoni nazo zimekuwa ni finyu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona katia taarifa ya bajeti hii kwamba mmetenga milioni 300 kwa ajili ya kulipa fidia, fedha hizi ni ndogo sana. Mwende mkaangalie jinsi gani ya kuweza kufanya. Lengo letu na kusudio letu mfanye kama ilivyofanyika pale kwenye Daraja la Nyerere, kuwe na njia saba za kuingilia na njia saba za kuweza kutokea na hii itasaidia sana. Muangalie vile vile jinsi gani ya kuweza kufanya kuhakikisha kwamba tunakuwa nae neo la ku–park. Si kila mtu anataka kuvuka na gari. Nilikuwa natamani kuona kwamba kuna sehemu ya parking ambayo mtu anaweza aka–park gari yake akavuka akaenda mjini kwa sababu kuna watu wengine wanaofanya kazi pale maeneo ya Kivukoni haitaji kuvuka na gari Kwenda mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ukishatoka kwenye kivuko upande wa kushoto ni eneo la bandari, hii ni Taasisi mama na sisi dada na TEMESA. Mimi nadhani suala hili liko ndani ya Wizara yenu, naomba mkae muangalie jinsi gani ya kufanya mawasiliano ili eneo ambalo halitumiki kwa upande wa bandari baada ya kuvuka upande wa kigamboni basi liweze kutumika katika sehemu ya park and go.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nitoe ushauri kwa Mheshimiwa Waziri, TEMESA ni Taasisi ambayo inasimamia masuala ya ufundi umeme na masuala ya vivuko. Mimi ushauri wangu, tuwekeze katika Nyanja ambazo tunaona zinakwenda kuwa na tija. Sasa hivi TEMESA Imejitawanya sana katika masuala ya mechanical, masuala ya electrical pamoja na masuala ya vivuko. Tukiweza kuijengea uwezo vizuri TEMESA katika masuala ya ufundi wakaweza kufanya matengenezo ya magari yote nchini, kwa maana ya magari ya Serikali, jukumu hilo peke yake linawatosha sana. Lakini vilevile wakatoa ushauri katika masuala ya umeme tukawanunulia vifaa, tukawapatia nyenzo za kuweza kufanya kazi. Majukumu haya yanatosha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado mimi kama Mbunge nitaendelea kusimama na kusema kwamba suala la vivuko liondolewe TEMESA. Wapeni watu wenye uwezo waende wakaifanye hiyo kazi. Wananchi wa Kigamboni wanahitaji usafiri wa uhakika ili wasafiri salama. Sasa hivi kutoka Kigamboni sehemu ambayo straight haifiki hata kilomita moja watu wanasubiria Zaidi ya saa moja. Tunataka ifike mahali ambapo mwananchi akifika pale dakika tano yuko upande wa pili wa mjini. Kwa hiyo nitaendelea kusisitiza kwamba huduma za vivuko zibinafsishwe. TEMESA ibaki na majukumu ya msingi ya huduma za umeme na ufundi na hao mkiwawezesha vizuri wataweza kufanya vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nilikuwa nataka nilisemee ni suala la miundombinu ya barabara. Katika wilaya za Mkoa wa Dar es Salaam Wilaya ya Kiagamboni ndiyo wilaya pekee katika Mkoa wa Dare es Salaam ambayo iko nyuma sana katika miundombinu ya barabara. Katika miundombinu ya barabara za TANROADS tuna asilimia 37 tu; na zaidi ya asilimia 50 ya barabara zote za TANROADS katika Mkoa wa Dar es Salaam ambazo hazijawekwa lami ziko katika Wilaya yetu ya Kigamboni. Tumechelewa sana na tuko nyuma sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigamboni ni Wilaya ambayo inakuwa kwa kasi kubwa mno. Sasa hivi uwekezaji wa viwanda ni mkubwa, kasi ya ujenzi ni kubwa, na Kigamboni ndilo eneo pekee ambalo sasa hivi vinapatikana viwanja vingi sana, na hata nikiangalia hapa ndani ya Bunge lako la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nina Wabunge nadhani theluthi moja kama si zaidi ni wakazi wa Kigamboni. Wamejenga au wana nyumba kule Kigamboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe sana Wizara ya Ujenzi iweke msukumo katika miundombinu ya barabara. Sasa hivi barabara ya kutoka Gomvu Kwenda Pembamnazi tulikuwa tumeijenga kwa kilomita moja moja ni ndogo sana. Kumekuwa na ujenzi mkubwa wa viwanda katika maeneo ya Kimbinji na tumetenga eneo la uwekezaji kule Pembamnazi, na hata Wizara ya ardhi imepima viwanja kule lakini watu wanashindwa kujenga kwa sababu hakuna miundombinu ya kuweza kufika kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Barabara ya Kibada – Mwasonga kueleke Kimbiji na Tundusongani, hili nisipolisema kwa kweli wananchi wa Kigamboni hawatanielewa. Barabara hii tuliipitisha katika bajeti ya mwaka jana, katika barabara chache ambazo Serikali iliridhia na tukaipitisha kwenye bajeti. Lakini nitoe malalamiko yangu makubwa sana, kwamba mchakato wa barabara hii umekwenda taratibu sana. Ni jana tu Mheshimiwa Waziri ndipo amekuja kunithibitishia, jana, kwamba tenda imefunguliwa juzi, Mkandarsi amepatikana. Na mimi nimemwambia Mheshimiwa Waziri jana, kwamba mchakato utakapokamilika aje yeye mwenyewe Kigamboni kutia saini ule mkataba na kuwaambia wananchi wa Kigamboni ujenzi unaanza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka umeniambia kwamba mkandarasi amepatikana, na tunategemea ndani ya mwezi mmoja ujenzi wa barabara mkandarasi wa barabara ya Kibada Kwenda Mwasonga atakuwa amepatikana. Nikutake Mheshimiwa Waziri uje wewe mwenyewe Kigamboni katika sherehe ya utiaji saini ya ile barabara ili na wewe useme na wananchi wa Kigamboni. Nimechoka kuwasemea kwa niaba yako, mchakato umekuwa ni mrefu sana, barabara hii tulipitisha kwenye bajeti ya mwaka jana, na sasa hivi imebakia mwezi mmoja kabla ya mwaka wa fedha kuisha. Kwa hiyo nikuombe sana, kabla ya mwaka huu wa fedha kwisha uje Kigamboni utie saini hii barabara. Umenithibitishia wewe mwenyewe kwamba mkandarasi ameshapatikana kwa hiyo ndani ya mwezi mmoja kamilisha hizo taratibu za mikataba ili uweze kuja kuwatangazia wananchi wa Kigamboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimuombe vilevile Mheshimiwa Waziri kuhakikisha kwamba hizi barabara nyingine especially ya Gomvu, Kimbiji mpaka Kwenda Pembamnazi nayo tunaiongezea wigo kuhakikisha kwamba nayo inafika Pembamnazi kwa sababu hili ni eneo la kimkakati na ni eneo la uwekezaji. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri wakati unapokuja kuhitimisha mimi nitaomba nipate commitment yako katika maeneo haya yote ambayo nimeweza kuyataja ili wananchi wa Kigamboni waweze kusikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana sana.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata dakika 10 na kwa kuwa ni mchango wangu wa kwanza ndani ya Bunge hili naomba niwasemee wananchi wa Kigamboni. Wananchi wa Kigamboni ili waweze kufika Mjini ni lazima wavuke maji. It is whether wapitie kwenye feri au wapitie kwenye daraja.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto kubwa sana sasa hivi kwa wananchi wa Kigamboni kutokuwa na uhakika especially pale panapokuwa na mahitaji yao kwenda Mjini. Vivuko vyote ambavyo vinafanya kazi pale MV- Magogoni, MV - Kazi na MV - Kigamboni vyote ni vibovu. MV - Kazi ambacho ni kivuko kipya kuliko vyote hivi sasa hivi kimetolewa kimepelekwa doc kwa ajili ya matengenezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoka Dar es Salaam hivi karibuni, juzi tu mimi mwenyewe nimejithibitishia nimekaa ndani ya maji zaidi ya nusu saa, kivuko kilikuwa kinazunguka, geti ya kufunguka haishuki, imebidi tutoe magari kwa kurudi reverse.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri alitembelea kivuko hiki cha MV - Kazi na aliahidi wananchi wa Kigamboni kwamba ndani ya muda wa miezi minne kivuko kile kitakamilika, hivi ninavyoongea matengenezo ya MV - Kazi hayajaanza, Serikali haijatoa fedha, nataka Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya hitimisho lake atuambie MV - Kazi inaanza kufanya kazi lini, fedha hizo zinatolewa lini, na ni lini wananchi wa Kigamboni wategemee kivuko kile kitaanza kufanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo usimamizi wa vivuko kwakweli ni mbovu sana, TEMESA wameshindwa majukumu yao. Ninaliomba Bunge lako kwamba sasa hivi wananchi wa Kigamboni pale ukiwahi sana kuvuka, ukifika pale ili uvuke ni dakika 45 hadi Saa Moja, leo hii asubuhi Nahodha wa MV - Kigamboni amekunjwa na abiria ambao walikuwa na jazba, kwa sababu amefika pale ameiweka Pantoni muda mrefu, wananchi wamekasirika wamemfuata kule kule kwenye Deck wameanza kupigana. Vivuko hivi vitakuja kuleta maafa, Mimi ninaomba kama TEMESA wameshindwa kazi tuvibinafsishe, wapewe watu wenye uwezo, waweze kuendesha vivuko hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili ni suala la daraja. Ninampongeza Waziri kidogo katika hili amewafuta machozi wananchi wa Kigamboni, lakini hoja ya wananchi wa Kigamboni ni kufuta tozo ya daraja. Daraja lile ni kiunganishi cha barabara ni sawasawa na madaraja mengine, inawezekana njia ambayo inatumika pale ni ya PPP hilo tunalielewa, lakini kuweka tozo pale inaongeza gharama sana kwa wananchi wa Kigamboni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa wa Kigamboni wanachangia katika ujenzi wa madaraja mengine nchini na wanachangia kulipa madaraja mengine nchini, iweje wananchi wa Kigamboni katika daraja linalowahusu wao walipe na Tanzania wengine wasichangie katika hili? Kwa hiyo nikuombe na Waziri hapa ananisikia, tumeanza hili la mwanzo bado tunahitaji tozo ya daraja la Kigamboni ifutwe ili kuwe na uwiano na madaraja mengine. Wananchi wa Kigamboni wanasema hawahitaji daraja la Tanzanite liwekewe tozo, tukiweka tozo katika daraja la Tanzanite tunajenga presidency mbaya, tutajenga presidency kwamba Kigongo Busisi ambalo linakamilika nalo tuweke tozo, tujaweka presidency kwamba daraja la mto Wami nalo tuweke tozo na tutarudi katika madaraja yote Tanzania tuweke tozo, tunasema kwamba madaraja ni viunganishi na Serikali ibebe gharama ya madaraja yote nchini (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu namba tatu ni suala la miundombinu ya barabara, Naibu Spika nawe ni Mbunge wa Dar es Salaam tunayo changamoto kubwa sana ya miundombinu ya barabara katika Wilaya za Dar es Salaam. Wilaya yangu ya Kigamboni ni moja ya Wilaya ambayo imekuwa na changamoto kubwa sana ya miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua katika bajeti hii tumetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Kibada - Mwasonga kwenda Tutisongani kwa kilometa 41 tunalipokea kama wananchi wa Kigamboni, lakini rai yangu kwa Wizara ya Ujenzi pamoja na TANROADS ni kuhakikisha kwamba hiyo barabara ambayo ni barabara ya kimkakati ambayo inakwenda kuchechemua uchumi wa Wilaya ya Kigamboni na Industrial Hub ambayo Mheshimiwa Rais alikuja kuizindua, basi hiyo barabara iweze kutengenezwa na tuweze kuijenga kwa ukamilifu wake wa kilometa zote 41. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo ninawaomba tena Wizara ya Ujenzi kuna barabara pacha ya kutoka Feri - Mji Mwema kwenda Pemba - Mnazi nayo tumekuwa tunaijenga kwa kilometa moja moja ingependeza hii barabara nayo kwa sababu inakwenda kuunganisha eneo la Pemba Mnazi ambako tumeweka ekari zaidi ya 1,000 za uwekezaji ili sasa na hilo eneo tuanze kulitumia katika masuala ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo niongelee changamoto ambayo wanaipata watumiaji wa barabara au watumiaji wa daraja la Nyerere. Katika barabara ya kutoka Bendera Tatu kwenda Darajani kuna mizani ambayo mmeiweka pale ambayo magari yakitoka bandarini yanapita kuangalia uzito kabla hayajaendelea. Ile mizani haitumiki kwa ajili ya kutoza faini au vitu vingine lakini inaleta msongamano usiokuwa wa lazima. Ninaishauri Wizara ya Ujenzi ule mzani muuondoe pale kwa sababu unaondoa maana nzima ya daraja ambalo lipo pale na kuongeza msongamano usiokuwa wa lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo mnafanya ujenzi wa mwendokasi, mnafanya ujenzi wa flyover pale karibu na Uwanja wa Taifa lakini Wakandarasi wale hawajaweka miundombinu mizuri ya michepuo hali ambayo inapelekea kuwa na foleni kubwa sana. Watumiaji wa Mbagala, wote wa Mkuranga sasa hivi wanapita Kigamboni, ninawaomba sana Wizara ya Ujenzi hakikisheni tunakuwa na barabara nzuri za michepuo na kuondoa ule mzani pale karibu na bandarini ili njia za kwenda na kutoka darajani ziweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa ninaomba LATRA ipo chini ya Wizara ya Ujenzi, mwananchi wa Kigamboni ili afike mjini anahitaji nauli tatu hadi nne. Akipitia kwenye kivuko anatoka kule alikotoka anavuka nauli ya pili anatoka pale anakwenda posta nauli ya tatu anakwenda sehemu ambayo anataka kwenda hiyo nauli ya nne, akipitia darajani anahitaji nauli tatu, ninawaomba LATRA kwa kuwa tozo za daraja zimepungua kwa kipindi hiki, tunatarajia kuona kwamba tutakuwa na route ndefu kama maeneo mengine ya Mkoa wa Dar es Salam, ambapo wananchi wanaweza kusafiri kwa kutumia nauli moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamuomba Waziri wa Ujenzi atakapokuja kufanya hitimisho aje na majibu ya hoja ambazo nimezieleza la sivyo nitasimama na kukamata Shilingi, kwa kipindi hiki naomba aje na hayo majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia katika mada ambazo zimewasilishwa siku ya leo. Na mimi nitajielekeza katika kuchangia wasilisho linalohusu Taasisi hii ya Dawa Afrika (African Medicene Agency).

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema kwamba naunga mkono azimio hili lipitishwe na Bunge lako tukufu. Dawa ni kitu muhimu sana katika tiba za binadamu lakini dawa vile vile ni siasa, dawa ni biashara. Na katika matumizi ya dawa kuna watu wana nia njema na wengine na nia isiyokuwa njema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu ambao wanatengeneza dawa bandia na watu ambao wanatengeneza dawa ambazo hazina ubora unaotakiwa. Kwa hiyo, Azimio hili linakwenda kuwezesha Nchi Wanachama kuweka mfumo mzuri wa kuweza kudhibiti bidhaa za tiba, kwa kuhakikisha kwamba dawa zinakuwa zina ubora, zenye ufanisi na usalama unaojitosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza sana Serikali ya Tanzania katika masuala ya udhibiti wa dawa tuko vizuri na Taasisi yetu ya TMDA inafanya vizuri sana. Hongera sana Mheshimiwa Waziri na timu yako, kwa usimamizi mzuri ambao unaufanya katika Wizara hii, ambao umepelekea Tanzania tunasifika katika masuala ya udhibiti wa dawa na vifaa tiba katika Bara la Afrika na dunia nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nini manufaa ya Mkataba huu? Kwanza, unakwenda kuboresha masuala ya mifumo ya udhibiti katika Bara letu la Afrika. Sambamba na hilo, litasaidia sana kuweka mfumo wa kuweza kubadilishana taarifa na kuweza kujengeana uwezo katika nchi zetu za Bara la Afrika. Pia sambamba na hilo, kila nchi ya Afrika ina mifumo yake ya udhibiti na usajili wa dawa. Azimio hilo litakwenda sasa kuweka mfumo mzuri wa kuweka viwango na vigezo ambavyo vitatumika katika Bara zima la Afrika. Hii itapelekea kuweka sasa mifumo ambayo inafanana na kuwavuta wale ambao wako chini na sisi ambao tuko katika viwango vya juu kwenda viwango vya juu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoka kusema hapa katika viwango vile vya kimataifa vina hatua nne. Sisi Tanzania tuko katika hatua ya tatu, ni jambo la kujivunia sana kama Watanzania. Naamini kwa kupitisha Azimio hili, litatusaidia hata sisi katika viwanda vyetu vya ndani, kupunguza mlolongo wa usajili na pale ambapo tutahitaji sasa bidhaa zetu kuzipeleka nje ya nchi, sasa hivi Tanzania tuna Viwanda vya Dawa takribani 18. Mfumo huu utasaidia sana bidhaa zetu kuweza kuuzwa nje ya nchi na kupunguza mlolongo wa usajili. Utaratibu uliopo sasa hivi ndani ya nchi yetu kila dawa tiba ni lazima isajiliwe na mlolongo wake haupungui miezi sita. Utaratibu huu utasaidia kuweka benchmarks nzuri ambazo naamini nazo zitasaidia sana katika udhibiti, vile vile katika suala la usajili wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nataka niweke angalizo moja. Sisi kama nchi tumefanya vizuri sana. Mifumo yetu iko vizuri sana katika suala zima la usajili na udhibiti wa dawa katika nchi yetu. Sasa ni muhimu sana wakati tunapitisha azimio hili, kuhakikisha kwamba taasisi yetu ya TMDA inaendelea kufanya majukumu yake ya kimsingi bila kuathirika na vipengele ambavyo vinaweza vikasababisha taasisi yetu na sisi kushuka chini, kwa sababu wote hatuko katika viwango vya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini kwamba, kwa kupitisha azimio hili Taasisi yetu ya TMDA ndiyo itakuwa kinara cha kusaidia nchi nyingine za Afrika na wao waweze kufikia katika viwango vya juu vya udhibiti wa ubora wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuomba jambo moja. Hili nitaendelea kulisema, lipo nje hapa kidogo, lakini tunaongelea masuala ya udhibiti wa vyakula. Katika nchi nyingi duniani suala la udhibiti wa dawa linakwenda sambamba na udhibiti wa usalama wa chakula. Suala la usalama wa chakula ni suala la afya, siyo suala la viwanda wala la biashara. Usalama wa chakula linapotokea changamoto katika suala la usalama wa chakula, uwe ni mlipuko wa magonjwa ambao umesababishwa na chakula, Wizara inayoshughulika ni Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tulihamishe hili jukumu kutoka Wizara ya Afya kwenda Wizara ya Viwanda na Biashara. Niwaombe sana, katika nchi nyingi mamlaka zinaitwa FDA (Food Drug Authorities), siyo Medical Authority. Kwa hiyo, niendelee kuiomba Serikali iende ikaliangalie suala hili, ikiwezekana suala la usalama wa chakula lirejeshwe chini ya TMDA ili sasa jukumu hili liweze kufanyika. Hili nalisema kwa sababu gani? Sasa hivi kuna uingizaji mwingi wa chakula na vyakula vingine havina ule ubora ambao unatakiwa. Najua kwamba TMDA…

MHE. ASKF. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa taarifa tu anayezungumza. Ni kweli kabisa kwa sababu, genetic modified food au chakula ambacho kimetengenezwa ku-genetic, ni hiyo hiyo sayansi ya dawa. Kwa hiyo, ikiwa pamoja itarahisisha sana kulinda watu wetu. (Makofi)

MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima kwa kuunga mkono hoja yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kwamba, pamoja na kukubali Bunge lako liweze kuliridhia Azimio hili, basi naliomba Bunge lako vile vile litafakari kurejesha majukumu ya usalama wa chakula chini ya Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wa Mwaka 2016
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kupata fursa ya kuchangia, lakini nianze kwa kusema kwamba nilitarajia kwamba schedule of amendments ya muswada unaohusu Chief Government Chemist Authority uwepo hapa ili na sisi tuweze kukaa na kupitia kuona yale marekebisho ambayo Serikali imeyafanya kupitia Kamati ambazo tulikuwa tumekaa imezingatiwa. Sasa niiombe Serikali watusaidie kupata amendments ili sasa na sisi tuweze kufuatilia kuangalia kwamba yale tuliyokuwa tumeyasema yameweza kufanyiwa kazi, hilo lilikuwa la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wa Chief Government Chemist kwa kuja na huu muswada na nina amini umekuja katika muda muafaka sana hususani wakati fani hii ya kemia inazidi kukua. Niseme tu kwamba ni mdau na ni mjumbe katika kamati ya huduma ya Jamii na Maendeleo ya Jamii. Ni kweli kabisa kwamba Chief Government Chemist alikuwa anadandia katika sheria za watu wengine. Kwa hiyo, sasa hivi sheria hii inakuja katika muda muafaka kuanzisha amakuwa na sheria ambayo itakuwa inasimamia taasisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali.
Vilevile itakuwa ni vizuri muswada huu mwingine ambao umekuja muda muafaka lakini vilevile umekuja sambamba na huu wa taasisi ni huu ambao unakuja sasa kuanza kusimamia taaluma ya wakemia nchini na hii ni hatua kubwa sana na ambayo kwa kweli tunataka tuipongeze sana Serikali na ukizingatia mkemia namba moja ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, naamini sheria hii itakapoanza baada ya yeye kusaini na ninyi mtamuomba ajisajili kama mwana taaluma katika fani hii ilikuendelea kuhamasisha fani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba ni Mjumbe katika Kamati, mapendekezo yetu tuliyatoa katika taarifa ambayo niliisoma asubuhi. Kwa hiyo, nitaongelea mambo ya ujumla kwa sababu mapendekezo na ndio maana nilikuwa nataka kuiona schedule of amendments kama yanazingatia yale ambayo tuliyasema katika Kamati. Sasa kwa sababu hiyo schedule haipo hapa nitajikita katika maudhui tu ya jumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ni ushauri wa ujumla na hii na yenyewe ni ka upande wa Serikali. Nadhani sasa hivi tunapokwenda huko mbele tujaribu kuangalia bodi badala ya kuwa ni za uteuzi tujaribu kuangalia kama tunaweza kutoa fursa watu wakaomba. Tuweke sifa na vigezo, tuwaachie Watanzania waombe; kuwe competitive na tuangalie watu kutegemeana na competency zao badala ya utaratibu wa sasa hivi ambao tunakwenda nao ili tuweze kupata watu wazuri katika hizi bodi ambazo wanaweza kutushauri katika taasisi zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka niligusie ni kuhusiana na utendaji kazi wa taasisi hii ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Ni taasisi muhimu na taasisi nyeti sana, lakini ina mchango mkubwa sana hususani katika makosa ya jinai, na moja kati ya jambo ambalo limekuwa likilalamikiwa sana ni ucheleweshaji na wazungu wanasema justice delayed is justice denied. Kwa hiyo, tuwaombe wenzetu waendelee kujipanga vizuri kuhakikisha kamba huduma hizi hususani katika vile vipimo ambavyo vinahusiana na kesi za jinai vinaharakishwa na kufanyika kwa haraka ili sasa wale ambao wanategemea haki kutokana na vipimo hivyo waweze kuvipata.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la tatu katika hili ambalo nilikuwa nataka kushauri kwa sababu tuna maabara nyingi na tumesema maabara hii itakuwa ndio supreme and referral katika masuala ya uchunguzi. Ni muhimu sasa tukauhisha majukumu ya maabara hii na maabara nyingine ambazo zipo chini ya Mkemia Mkuu wa Serikali zikawa na mahusiano pamoja na mawasiliano na hususani hapa nilikuwa nalenga maabara nyingine kama za Jeshi la Polisi ambao nao wana forensic laboratory yao. Ni kuangalia jinsi gani ambapo wanaweza kufanya kazi kwa pamoja pasipo kuleta migongano, ni kuangalia ni jinsi gani wanaweza kufanya kazi kwa pamoja na maabara ya TFDA, maabara za TBS, maabara nyingine za Wizara ya Maji na taasisi nyingine zote ambazo zina maabara ili kuleta ufanisi na kujenga mahusiano yaliyokuwa mema na kuondoa duplication katika kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mengine nilitaka kugusia ni masuala tu ambayo yapo katika jamii yetu. Sisi ambao tunaishi Dar es Salaam mboga nyingi zinalimwa katika Bonde la Mto Msimbazi na katika Bonde la Mto Msimbazi pale hatuna uhakika sana na usalama wa maji ambayo yanatumika kunyweshea zile mboga. Tulikuwa tunaiomba sana Serikali itutoe mashaka wana Dar es Salaam lakini watutoe mashaka wakazi wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na wananchi kwa ujumla kwamba mboga tunazokula za kutoka Bonde la Msimbazi zipo salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile tumekuwa na changamoto hususani katika uhifadhi wa nafaka ndani ya maghala ya Taifa, lakini vilevile katika maghala ya watu binafsi, tumekuwa na changamoto kubwa sana kuhusiana na uhifadhi wa nafaka. Ni muhimu sana maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ikawa proactive badala ya kuwa reactive kuhakikisha kwamba hizi nafaka ambazo zipo katika maghala yetu nazo zipo salama. Isijekuwa tunatoka kwenda kushuhudia matukio ama kushughulikia matukio wakati tungeweza kufanya kazi ya kuzuia matukio. (Makofi)
Mwisho mimi niipongeze Serikali sana, Mheshimiwa Ummy Mwalim, Mheshimiwa Dkt. Hamis Kigwangalla, Profesa Manyele, Mwenyekiti wa Bodi ya Mkemia Mkuu - Profesa David Ngasapa, mwalimu wangu kwa kazi kubwa sana ambayo wameifanya kuhakikisha kwamba miswada hii inakuja kwa muda muafaka, tunakuwa sasa na sheria ambayo itaisimamia chombo hiki, sheria mbayo itasimamia taaluma hii. Na nina hakika kabisa sheria hizi zikishapitishwa basi taasisi hii inaweza ikasimama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimalizie na sisi kama Wabunge tunaomba tuwaunge mkono taasisi hii na sisi kuhakikisha kwamba tunapigia debe waweze kupata fedha za kutosha kwa ajili ya kuendesha taasisi hii. Nashukuru sana.