Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Esther Nicholus Matiko (125 total)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwenye swali langu la msingi nimeelezea dhahiri kwamba hospitali ya Mji wa Tarime inatoa huduma kwa Wilaya nzima ya Tarime na baadhi ya wananchi wa Serengeti na Wilaya ya Rorya. Serikali imekuwa ikileta fedha za OC na bajeti ya dawa, kwa kufuata population ya Mji wa Tarime ambayo ni watu 78,000. Ppia imekuwa ikileta, fedha la kapu la pamoja kwa maana ya basket fund, milioni 106 tu ambayo haikidhi haja na zamani tulikuwa tukipokea zaidi ya milioni 500 bado huduma za afya zilikuwa siyo dhahiri.
Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwa nini Serikali sasa, isiweze kuleta fedha za OC na za basket fund kwa kufuata population walau ya Tarime Rorya na siyo ya Mji wa Tarime, ukizingatia kwamba tunatoa huduma kote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wanaopata huduma ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, wamekuwa wakitozwa sh. 6,000 lakini wakifika ndani hawapati madawa, hawapati huduma zinazostahili, ni kwa nini sasa Serikali kwa maana katika Hospitali ya Mji wa Tarime tayari tuna jengo ambalo liko tayari, kuweza kufungua duka la dawa kwa maana ya MSD ni kwa nini sasa Serikali isiweze kuja na kufungua hilo duka pale kwenye hospitali ya Mji wa Tarime ili wananchi waweze kupata huduma ya madawa wanavyoenda kutibiwa pale kuliko kuhangaika tena wanatoa sh. 6,000 halafu akitoka nje anaambiwa hamna dawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, swali la kwanza ni kwa nini Serikali, isichukulie takwimu kwamba Hospitali hii ya Mji wa Tarime inatibu pia wateja kutoka Rorya na maeneo mengine ya jirani. Jibu ni kwamba Serikali siku zote inapopanga Mpango wake wa Bajeti kwa ajili ya kuzihudumia hospitali zote nchini ina formula maalum ambayo inazingatia kigezo anachokisema cha idadi ya watu wanaohudumiwa katika hospitali. Pia, pesa zote zinazotoka kwa wafadhili zinapangwa kwenye bajeti kutokana na burden of desease, mzigo wa magonjwa ambao unahudumiwa katika eneo la kijiographia ambapo hospitali hiyo inatoa huduma.
Kwa hivyo, watu wote wanaofanya planning kwenye sekta ya afya, wanazingatia kigezo cha idadi ya watu, lakini pia mzigo ambao hospitali husika inaubeba kwa maana ya kutoa huduma zake. Kwa maana hiyo, niseme tu maelezo ya ziada hapa kwa Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika, kwamba changamoto ya kuwahudumia Watanzania kwenye eneo hili la dawa, vifaa na vifaa tiba ni kubwa sana, kwa maana ya mzigo wa kibajeti ambapo Sekta ya Afya inabeba. Changamoto hiyo itaweza kutatuliwa kwa jitihada ambazo tunazifanya sasa hivi za kuhakikisha Watanzania wote wanakuwa na bima ya afya, hili ni jambo ambalo lipo kwenye Ilani ya Uchaguzi pesa tulizonazo sasa ni ndogo haziwezi kubeba mzigo wa kutibu Watanzania wote kama ambavyo tunatamani iwe, sasa tunakuja na jitihada mpya ya kuhakikisha Watanzania wote wanaingia kwenye Mfuko wa Bima ya Afya ili hospitali zenyewe ziweze kukidhi mahitaji ya madawa, vifaa tiba na vitendanishi kama ambavyo zinajipangia.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu duka la dawa la MSD. Nimpongeze Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko na wataalam wetu wa sekta ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, kwa kuandaa eneo kwa ajili ya kuanzisha duka la MSD. Kwanza nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa kuanzisha mkakati, wa kufungua maduka ya MSD yaani MSD Community outlets.
Maduka haya kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais yanatoa huduma kwenye hospitali ya Taifa na hospitali za Kanda kwa maelekezo yake, lakini kwa kuzingatia mahitaji ya Mikoa na Wilaya zote nchini kwamba wangependa kuwa na maduka ya MSD, ili waweze kuhakikisha wananchi wanapata dawa kwa ukaribu na kwa gharama nafuu zaidi, ndani ya hospitali kuliko kuzifuata nje ya hospitali. Wizara yetu imewaelekeza MSD waandae Mpango Mkakati wa kutoa utaalam wa kiufundi wa namna ya kuanzisha maduka ya dawa, katika mfumo huu wa MSD community outlets. Taasisi yetu ya MSD, imejipanga kuwasaidia Milkoa.
Pia Taasisi yetu ya NHIF imejipanga kuingia kwenye mkakati wa kuwakopesha hospitali yoyote ile iwe ya Mkoa ama ya Wilaya, fedha kwa ajili ya kuanzisha maduka haya na MSD itatoa technical support, ikiwepo mifumo ya kuendeshea maduka haya kama mifumo ya computer ili kuweza kuyaendesha kisasa zaidi na katika mtindo ule ule ambapo maduka yetu ya MSD community outlets yanaendeshwa.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa masikitiko makubwa sana nimefedheheshwa na majibu ya Wizara kwa sababu amenijibu kuhusiana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na mimi nimeuliza kuhusiana na Halmashauri ya Mji wa Tarime ambapo Mnada wa Magena upo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu, kwa kuwa katika majibu yao ambayo hayajakidhi wametamka dhahiri kwamba walifunga mnada huu kwa sababu za wizi wa ng’ombe na usalama. Kwa kuwa Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi imeanzisha Kanda Maalum ya Tarime - Rorya ambapo hivi sasa usalama umeimarika ingawa bado wanaongelea suala la wizi. Vilevile wameainisha kwenye majibu yao kwamba 1996 tu waliweza kupata Sh.260,000,000 na sasa hivi 2015 wanapata Sh.212,000,000, hawaoni kuwa Serikali inapoteza mapato mengi sana kwa kutokuanzisha ule mnada ambao ulikuwa umeshajengwa ambapo kwa sasa hivi unaweza kupata zaidi ya Sh.1,000,000,000? Hilo ni swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni dhahiri kabisa na hata kwenye majibu yao wamesema Mnada wa Mtana, Kewenja, Nyamwaga na Chemakolele ipo katika Halmashauri ya Wilaya na ni dhahiri kabisa pia kwamba huu mnada ulihamishwa kwa sababu za kisiasa kwa sababu huwezi ukasema Kirumi ipo mpakani na Kenya. Napenda kujua sasa ni lini Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi itaacha siasa iweze kufanya mambo ya kimaendeleo na Mnada wa Magena ufunguliwe ili wananchi wa Tarime wafaidike? ((Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kupoteza mapato, ni kweli kabisa kuna changomoto kwamba Serikali ingeweza kupata mapato mengi zaidi kwa kuendelea na mnada ule. Hata hivyo, katika hali iliyopelekea mpaka mnada husika ukafungwa, ukweli wa mambo ni kwamba hata kukusanya mapato ilikuwa haiwezekani. Kwa sababu Serikali ina jukumu la msingi la kulinda amani na usalama, kwa kweli ilikuwa haiwezi kuendelea kuruhusu mnada ule utumike wa sababu watu mali zao zilikuwa zinapotea na walikuwa wanatishiwa maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, hakuna shughuli za kiuchumi ambazo zilikuwa zinaenda kama ilivyotarajiwa. Kwa hiyo, pamoja na kwamba ingeweza kupata mapato lakini haikuwezekana kuendelea kuwa na shughuli yoyote katika hali ambayo si salama. Hata yeye mwenyewe amekiri kwamba kulikuwa na hali ya kutishia amani na usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mnada husika kufungwa na mwingine kuanzishwa kisiasa, nimhakikishie tu Mheshimiwa Matiko kwamba kilichopelekea mnada huu kufungwa na mwingine kuanzishwa siyo sababu za kisiasa ni kwa sababu ulinzi na usalama wa wananchi wa Tarime ulikuwa ni wa muhimu zaidi. Vilevile nimhakikishie tu kwamba kwa hali ya sasa mnada ule mpya unafanya kazi kama ile iliyokuwa inafanywa na mnada wa awali. Cha maana ni wananchi kupata fursa ya kuuza mifugo yao kwenda nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama kuna mnada ambao unafanya kazi ileile vizuri zaidi na hauhatarishi usalama, kwa vyovyote vile Serikali itachukua uamuzi wa kuhakikisha kwamba mnada huo unaendelea badala ya kufikiri kwamba ni lazima kurudi kwenye mnada ambao kwa kweli uendeshaji wake ulikuwa unatishia ulinzi na usalama.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kweli majibu yaliyopatikana leo, ni dhahiri kabisa hata Serikali haijui mipaka ya Kata. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amekiri kwa kinywa kwamba wanatwaa ardhi kwa kufuata Sheria ya mwaka 1999 na kwa kuwa JWTZ hawakufuata sheria, mwanzoni waliomba hifadhi ya miezi mitatu katika Kata ya Nkende, walivyopewa wakaamua kuhodhi na Kata ya Nyamisangura na Nkende na Nyamisangura, siyo eneo la Nyandoto. Kikosi cha Jeshi kinatakiwa kukaa Kata ya Nyandoto na siyo Nyamisangura na Nkende.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa sababu hawakufuata Sheria ya mwaka 1999, kama alivyotamka mwenyewe, haoni sasa kwamba ni dhahiri wananchi hawa wanatakiwa kuhodhi maeneo yao kama mlivyoyateka mwaka 2008 mpaka sasa hivi, mwaache waendeleze shughuli zao za kiuchumi?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Waziri anasema kwamba wanaenda kukamilisha utathmini, ifahamike kwamba waliwazuia wananchi hawa kufanya shughuli za maendeleo kuanzia mwaka 2008, hawafanyi shughuli zozote za maendeleo. Sasa hiyo tathmini ambayo Waziri anakiri kwamba anaenda kuikamilisha mwaka huu, napenda kujua na wananchi wa Tarime wajue kwamba mtazingatia hali halisi ya mwaka 2007, ambapo Wanajeshi hao waliwakataza wananchi wasifanye shughuli zozote za maendeleo; nyumba zimebomoka, vyoo vimebomoka, mashamba yameshakuwa chakavu sasa hivi ni ardhi tu; huo utathmini ambao mnaenda kuufanya sasa hivi, unazingatia vigezo vipi? Ahsante.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunakiri kwamba wananchi walizuiliwa kuendelea na shughuli za uchumi kwa sababu ya kuweka Kiteule cha Jeshi.
Napenda Mheshimiwa Mbunge aelewe kwamba amani na usalama katika eneo nalo ni muhimu kwa ajili ya shughuli za uchumi. Kwa hiyo, maelewano yalifanyika kwamba wananchi wapishe Jeshi hapo kwa ajili ya shughuli za usalama ili na wao waweze kupata fidia.
Kwa hiyo, hatua tuliyofikia ni nzuri naweza nikasema, kwa sababu sasa tunasema kwamba fedha za uthamini zimeshapatikana na zimeshatumwa kwenye Halmashauri. Ni jukumu la Halmashauri kukamilisha uthamini ili wananchi hao waweze kulipwa fidia inayostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu tathmini kuchukua viwango vya mwaka 2007 au sasa, kwa mtazamo ni kwamba viwango vya sasa vitakuwa vikubwa zaidi kuliko mwaka 2007.
Kwa hiyo, tunachosema tu ni kwamba, kwasababu uthamini huu unafanywa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya, ni vyema Mheshimiwa Mbunge ukashirikiana na Halmashuri yako pamoja na watendaji wa Wizara yangu ili kuweza kupata tathmini stahiki bila ya mtu yeyote kuonewa. Kama kweli kuna nyumba ambazo zilikuwepo ambazo zimebomoka, tutalizingatia hilo ili kila mtu aweze kupata fidia yake anayostahili.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba, posho za Madiwani kwa maana ya vikao na posho za Wenyeviti wa Mitaa, Vitongoji na Vijiji zinalipwa na Halmashauri na kwa kuwa Serikali imekiri kabisa kwamba wanatambua kuna Halmashauri zingine hazina uwezo, makusanyo ya ndani ni madogo kama ilivyo Halmashauri ya Mji wa Tarime.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini sasa Serikali isione ni vema mathalani kwenye vikao vya Madiwani ambavyo tumeona vinatofautiana kati ya Halmashauri moja na nyingine, wengine wanalipwa 60,000, wengine 80,000 wengine 250,000 wengine 300,000, kwa nini wasi-standardize iwe kama tunavyolipwa posho Wabunge kwa Tanzania nzima na iweze kutenga fedha, isitegemee mapato ya Halmashauri ili Madiwani wanavyokaa vikao vyao waweze kulipwa fedha ambazo ni uniform kwa Tanzania nzima, vilevile kwa Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kuhusuiana na suala la Wenyeviti wa Mitaa na Vitongoji na Vijiji. Tumeshuhudia wananchi wakienda kupata huduma majumbani kwao. Serikali inajibu kwamba, inategemea mapato ya Halmashauri. Narudi pale pale tuna Halmashauri zingine mapato ni madogo sana na haiwezi kujenga Ofisi za Wenyeviti. Kwa mfano, kwangu Halmashauri ya Mji tuna Mitaa 81 Halmashauri ya Mji wa Tarime haiwezi ikajenga hizo ofisi. Kwa nini sasa Serikali isione umuhimu kuwapatia hawa Viongozi ofisi zao iwajengee, itenge fungu kutoka Serikalini ishuke chini kwenye Halmashauri zote nchini iweze kujengewa ofisi ili kuepuka adha ambayo inaweza kupelekea hata wengine kushawishika na kutoa na vitu vingine?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vitongoji lakini pia Wenyeviti wa Vijiji wanafanya kazi nzuri sana na kila mmoja anajua. Lakini pia ndiyo ambao wanazisaidia sana hizi Halmashauri katika kutekeleza shughuli zake ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa hayo mapato yenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, itakuwa ni jambo la kusikitisha na linashangaza na tutachukua hatua kali sana kusema ukweli kwa Halmashauri zote ambazo hazitaheshimu formular ile ya asilimia 20 ya mapato ya ndani kuzipeleka kwa hawa watu muhimu sana wanaowasaidia katika kutekeleza miradi lakini pia kukusanya mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali itahakikisha inalisimamia jambo hili, lakini tusaidiane Waheshimiwa Wabunge ninyi ndiyo Wajumbe wa Halmashauri zenu huko. Haya yanafanywa na watu ambao wako chini yenu kabisa kinidhamu, kwahiyo ni vizuri tukasikia huko mnachukuliana hatua kwa sababu mna hiyo mamlaka na sisi tukaja kusaidia pale tu ambapo huyu mtu amekuwa ni tatizo sugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vigumu pia kuweka standard formula na standard formula tulioiweka kama Serikali tumesema ni asilimia 20 ya mapato ya ndani, kwa sababu kwanza kabisa ili uweze ku-establish Halmashauri lazima vigezo kadhaa uweze kuvifikia ikiwa ni pamoja na hali ya uchumi wa eneo husika. Sasa tulipokuwa tunaomba Halmashauri, tunaomba tu ili tuweze kuzipata, lakini tunakuja kupata shida pale inapokuwa vigezo vile tulivyovisema siyo halisi kwa sababu huko kiwango cha uwezo wa ndani ndiyo unao-determine uanzishwaji wa Halmashauri husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi naamini kwa Halmashauri zilizoanzishwa na kama kweli zilikidhi vigezo vilivyopo kwa mujibu wa sharia, basi haziwezi zikashindwa kabisa kuweza kuwalipa posho hawa watu muhimu sana katika ngazi ya Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Mitaa. Kwa sababu hawa watu kama nilivyosema ndiyo wanaosaidia kukusanya mapato hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili juu ya ofisi za Viongozi hawa muhimu ni kweli tungeweza kusema ni jambo zuri kwamba nchi nzima tukawa na utaratibu wa kujenga ofisi hizi zote, lakini kama mnavyofahamu bajeti yetu ni hiyo moja na kupanga ni kuchagua, ndiyo maana tumeziachia Halmashauri kwa dhana ya kupanga vipaumbele vyao, basi kama kipaumbele cha Halmashauri fulani ni ofisi hizi tunaweza tukaanza na hizo na sisi Serikali Kuu tutatenga kwenye bajeti yetu kwa kadiri ya sealing ilivyopangwa kuhakikisha kwamba, tuna-facilitate au tuna-fund miradi ambayo imeibuliwa kutoka huko chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni jukumu la Halmashauri kuhakikisha kwamba kutokana na makusanyo yao ya ndani ambayo hayana masharti kutoka Serikali Kuu, basi wanapanga kupunguza upungufu huo wa ofisi kila mara wanapopanga katika bajeti zao.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Matatizo yaliyopo kwenye Kituo cha Afya cha Chamwino ni sawa sawa na matatizo yaliyopo kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime ambayo inahudumia takribani wananchi zaidi ya 500,000, hawana kifaa cha ultra sound. Ningependa kujua sasa ni lini Serikali itaona kuna umuhimu wa dhati kabisa wa kuleta huduma hii ya kifaa cha ultra sound kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime ili kuondoa hizi adha kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nimemsikia Mheshimiwa Esther, lakini katika jibu langu la msingi alishasikia pale awali. Mimi naamini kwamba ni kweli changamoto hii ni kubwa na ndiyo maana katika mwaka huu ukiangalia katika bajeti yetu ya TAMISEMI, development budget karibuni ni shilingi bilioni 182.5.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hiyo kuna sehemu zingine watu wameweka vipaumbele vya vifaa tiba, wengine wameweka magari ya wagonjwa, wengine wameweka miundombinu kujenga wodi za wazazi. Kwahiyo, japokuwa hii ni changamoto iliyopo pale Tarime naomba vilevile Waheshimiwa Wabunge tutumie fursa zinazowezekana katika mchakato wa bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ni kwamba mchakato wa bajeti wa mwaka huu ulivyokuja Wabunge wengi sana tulikuwa katika vikao vingine vya Kamati, inawezekana hiyo ndio ndo ikawa miongoni mwa changamoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini huko mbeleni tunapokwenda tuangalie jinsi gani tufanye ili michakato ya bajeti itakavyoendelea sisi Wabunge tuwe mbele kuwa main stakeholders katika ile budget process. Hii itasaidia vile vipaumbele ambavyo sisi kama Wabunge wa majimbo tunaona kwamba ni jambo la msingi kuwa katika bajeti yetu viweze kufanyiwa kazi.
Hata hivyo Mheshimiwa Esther Matiko nimelisikia jambo hili, tutawaambia wadau mbalimbali kuona ni jinsi gani wanaweza wakatusaidia. Lengo letu kubwa ni kwamba mwananchi katika kila angle katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aweze kupata huduma bora na mama aweze kunusurika katika suala zima la uzazi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Askari Magereza wapo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kwa kuwa Askari Magereza na wenyewe wanajiendeleza, wanapata shahada, wanapata elimu ya juu zaidi, lakini mishahara yao imekuwa ikibaki kuwa ile ile ambayo haitofautiani na askari wa kawaida aliye na cheti cha form four. Ukiangalia Jeshi la Polisi mtu mwenye shahada anapata sh. 860,000 lakini pia anapata posho ya ujuzi asilimia 15, kwa Askari Magereza wanalipwa sh. 400,000 wakikatwa inabaki 335,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua sasa ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuwalipa Askari Magereza kulingana na ujuzi wao maana imekuwa ikiwaahidi kwamba itawaongezea mshahara kulingana na ujuzi wao, lakini mpaka leo bado. Ni lini sasa itakwenda kuwalipa Askari Magereza kulingana na ujuzi wao ili kuwapa motisha kama askari wengine?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko hususan katika masuala mazima ya kupanga mishahara ya Askari Magereza.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua katika kada mbalimbali si wote ambao wanapata mishahara ambayo inaendana na kazi zao. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Esther Matiko, tayari tumeshaanza zoezi la tathmini ya kazi na hata ninavyoongea hapa watu wangu wa Bodi ya Mishahara wako hapa Bunge, wameshaongea na Tume ya Huduma za Bunge, lakini vilevile wameshazunguka nchi nzima kuongea na kada mbalimbali. Ifikapo mwezi wa Pili zoezi hili litakuwa limekamilika na baada ya hapo tukae sasa kupanga uwiano wa kazi pamoja na uzito wa majukumu kwa kada moja baada ya nyingine tukitambua ugumu wao wa kazi pamoja na majukumu yao. Vile vile tutaweza kupanga pia miundo yao pamoja na madaraja yao katika ngazi za mshahara. Kwa hiyo, nimhakikishie zoezi hili litaweza kufanyika kwa Askari Magereza, lakini vilevile kwa watumishi wote wa umma kwa ujumla wake.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa tatizo la maji lililopo Jimbo la Mpwapwa linaonesha uhalisia wa ukosefu wa maji Tanzania nzima likiwepo Jimbo la Tarime Mjini, na kwa kuwa maji safi na salama ni muhimu kwa afya za binadamu; ni lini sasa Serikali ya Chama cha Mapinduzi itaona kuna umuhimu wa kuwapatia maji wananchi wa Jimbo la Tarime Mjini maji safi na salama kwa kutekeleza bajeti ambayo tuliipitisha hapa, ambayo bado hamjaanza kuitekeleza mpaka sasa hivi, ili wananchi wa Tarime Mjini na Tanzania kwa ujumla waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokisema ni kweli, tatizo la maji sio Tarime tu, ni nchi nzima, na ndiyo maana katika mipango ya Serikali tumejielekeza jinsi gani tutafanya kuhakikisha tatizo la maji tuweze kulipunguza. Hata sasa hivi katika halmashauri zetu ukiangalia, takribani shilingi bilioni 25 zimepelekwa ili miradi ya maji iweze kufanyika katika hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwamba sisi dhamira yetu ya dhati ni kuhakikisha katika bajeti ta mwaka huu ambayo Serikali inafanya mpango, utaratibu mzuri wa kupeleka hizi fedha, utafikia mahali pazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Matiko asiwe na hofu katika hili, tutasimamia bajeti za Halmashauri, lengo letu ni kwamba ile bajeti ya karibu halmashauri zote na TAMISEMI, zaidi ya shilingi trilioni 6.4 ziweze kutekelezeka katika mwaka huu wa fedha. Na hili ni wazi kwa sababu mchakato wa ukusanyaji wa mapato unavyoendelea Serikali tuta-pump hizo pesa lakini sisi tuliopewa dhamana ya kusimamia tutahakikisha tunasimamia wananchi waweze kupata huduma ya maji.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Spika, kiukweli nasikitika kwa majibu ya Waziri wa Katiba na Sheria kuhusiana na umuhimu wa kuwa na Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Rorya. Tangu Bunge la Kumi nakumbuka nikiwa Mbunge wa Viti Maalum nimekuwa nikiongelea suala zima la kupatikana kwa Mahakama ya Wilaya ya Rorya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kukiwa hakuna Mahakama Wilaya ya Rorya, Mahakama ya Wilaya ya Tarime inakuwa na kesi nyingi na ndiyo maana mwisho wa siku tunakuwa na mrundikano wa kesi ambazo hazifanyiwi uamuzi kwa muda muafaka. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa sababu Rorya tayari wana ardhi na kwa sababu tumekuwa tukiongea umuhimu kuwa na Mahakama ya Wilaya ya Rorya tangu Bunge la Kumi, ni vegezo vipi ambavyo vilitumika kwa bajeti ya mwaka 2016/2017 wasipeleke Mahakama ya Wilaya Rorya wakaamua kupeleka sehemu nyingine Tanzania ikizingatiwa jiografia ya Wilaya Rorya ni kubwa, watu wanatoka mbali sana kuja Wilaya ya Tarime. Naomba kujua ni vigezo vipi vimetumika kwa Serikali isiweze kujenga Mahakama ya Wilaya ya Rorya mwaka huu wa fedha hadi waseme ni mwaka ujao wa fedha?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nimetamka mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba tuna tatizo kubwa la miundombinu ya mahakama, kuanzia Mahakama ya Mwanzo hadi Mahakama Kuu katika nchi yetu. Nimelieleza wazi hili na tatizo hili haliko Rorya tu!
Mheshimiwa Spika, nilimeshaeleza wakati ninajibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge watatu katika Mikutano iliyopita kwamba ninalishukuru Bunge lako Tukufu limetupitishia shilingi bilioni 46.76 kwenye Mfuko wa Mahakama na hizo shilingi bilioni 46.76, tutatumia shilingi bilioni 36 kujengea mahakama hii haijapata kutokea. Vilevile, tuna fedha ambayo mapema mwaka huu, mnakumbuka Mheshimiwa Rais aliagiza wapewe zote mahakama shilingi bilioni 12.3 jumla ni bilioni 48.3.
Mheshimiwa Spika, tumesema tunaanza kwa ujenzi wa mahakama 40 katika mwaka huu wa fedha, ninaomba utuamini kwa sababu mahakama sasa hivi imeshaanza ujenzi wa kisasa wa mahakama tena nafuu, lakini ujenzi uliyo bora kwa miezi mitatu anapata mahakama ya kisasa kama tulivyofanya mahakama ya Wilaya ya Kibaha.
Namuomba Mheshimiwa Mbunge avumilie tu, tumeipanga Rorya katika mwaka wa fedha 2017/2018, wavumilie kama Wilaya zingine zinavyovumilia kwa sasa.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naitwa Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko.
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kabisa kwamba ukosefu wa nyumba za walimu na kukaa mbali na shule unasababisha kutokuwa na kiwango kizuri cha ufundishaji kwenye shule zetu. Hivi karibuni tulisikia kauli ya Waziri Mkuu akitoa msisitizo kwamba walimu waishi kwenye shule ambazo wanafundisha. Kwa majibu ya Naibu Waziri ni dhahiri bado Serikali haijawa na mpango madhubuti wa kuhakikisha walimu wanakaa kwenye maeneo ambayo wanafundisha.
Ni nini mpango mkakati wa Serikali hasa kwa pale ambapo wananchi wamejenga maboma wanashindwa kuyamalizia ili watoto wetu waweze kupata elimu mbadala kwa Walimu kukaa maeneo ya shule. Napenda kupata mkakati ambao unatekelezeka siyo wa kuandikwa tu kwenye makaratasi, ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza na kuongezea kwenye swali la msingi pia ambalo limejibiwa na Naibu Waziri vizuri kabisa, Mheshimiwa Jafo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna mahitaji makubwa ya madarasa, tuna mahitaji makubwa ya nyumba za walimu. Kwa mfano, tuna upungufu wa madarasa katika shule ya msingi kwa sasa 127,745. Tuna upungufu wa madarasa kwa shule za sekondari 10,204. Hali kadhalika tuna upungufu wa nyumba za walimu. Mipango yote, mpango uwe mpango mkakati, uwe mpango wa haraka, uwe mpango wa dharura, inafanyika kwenye Halmashauri zetu. Tusitegemee kwamba tutakuja na mpango fulani nje ya mipango ile ya Halmashauri, kwa sababu Serikali kwa mujibu wa Katiba, kwa mujibu wa sheria, tunatekeleza dhana ya ugatuaji wa madaraka.
Mheshimiwa Spika, kugatua madaraka maana yake ni kwamba tupange vipaumbele sisi tulioko huko kwa wananchi. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kwanza kuwapongeza sana wananchi wote wa Tanzania wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, kwa namna tulivyoshirikiana vizuri sana katika suala la kupunguza upungufu wa madawati. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo sasa, tuangalie namna ya kwenda kwenye mchakato wa kupunguza tatizo la nyumba za walimu na madarasa. Tukifikiri kuna njia nyingine nadhani tutakuwa tunajidanganya, ukweli ni kwamba lazima tujipange wenyewe kwa kutumia rasilimali zilizopo na ndiyo maana katika bajeti ya mwaka huu tunayoiandaa, msisitizo mkubwa ambao tumeelekeza Halmashauri sisi TAMISEMI ni kwamba wajipange sana kuweka fedha nyingi na mipango mikubwa kwenye madarasa na nyumba za walimu. Hii itatusaidia ili hata Serikali kama ikitoa fedha yoyote ile, itakwenda kwa njia hiyo ili kutekeleza upungufu uliopo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Jimbo la Tarime Mjini lina kata nane na kati ya kata nane, kata nne ziko pembezoni na hazina umeme kabisa na kata mbili zina umeme kwa asilimia chache. Ningependa kujua commitment ya Serikali ya kuhakikisha kwamba wananchi wa Jimbo la Tarime Mjini wanapata umeme kwa asilimia zaidi ya 90.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Esther, tumeshirikiana naye sana kwenye mradi wa REA Awamu ya Pili na ni kweli kuna kata nne na kata nyingine mbili ambazo hazijaguswa kabisa. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Esther kwamba Jimbo lako pamoja na Mkoa wa Mara tumeshaanza kutekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu wa desification. Hapa ninapozungumza wiki ijayo mkandarasi ata-report kwake ili amwelekeze maeneo mahususi. Kwa hiyo, kata zake nne na zile tatu ambazo anazungumza Mheshimiwa Mbunge zitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu unaoanza mwezi wa Tatu na kuendelea.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru. Kwa kweli niendelee kusikitika kwamba Serikali inashindwa kuona barabara ambazo zinaweza zikaongeza chachu ya ukuaji wa uchumi kwenye nchi yetu kupitia utalii.
Mheshimiwa Spika, ningependa kujua ni lini Barabara ya Tarime – Nata kwa maana ya kwenda Mugumu itakamilika kwa kiwango cha lami? Mheshimiwa Naibu Waziri anatueleza
kwamba upembuzi yakinifu unakamilika 2018, watalii wengi wanaotoka Kenya wanapita Tarime wanaenda Serengeti, tukiboresha ile barabara kwa kiwango cha lami tutakwenda kukuza uchumi wetu kwa sababu watalii wengi watapita
kwa sababu barabara inapitika. Ni lini sasa Serikali itajicommit, isiseme leo itamaliza upembuzi yakinifu 2018, ione kuna uhitaji wa haraka sana wa kujenga barabara ya Tarime – Mugumu na iweze kumalizika ndani ya mwaka mmoja kama ikiwezekana tuweze kukuza uchumi wa nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA
MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, katika ujenzi wa barabara tuna hatua tatu muhimu na hatua hizi ni lazima zikamilike. Hatua ya kwanza ni upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Baada ya Serikali kuiona barabara hii kwamba ina umuhimu na inaongeza mapato yetu katika utalii imeamua kuianza hiyo kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kazi hiyo itakamilika mwaka 2018.
Mheshimiwa Spika, baada ya kazi hiyo kukamilika,
hatua ya pili itakayofuata ni kutafuta fedha za ujenzi wa barabara hiyo. Huwezi ukajenga barabara bila fedha. Kwa hiyo, Serikali itatafuta fedha ili tuanze kujenga barabara hiyo.
Tukishapata fedha tutatangaza tumpate mkandarasi wa kuanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nasikitika kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani leo hii inaita kwamba ni Wilaya ya Tarime/Rorya haijui kwamba ni Mkoa wa Kipolisi wa Tarime/Rorya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya masikitiko yangu, nipende kumwambia Naibu Waziri kwamba tayari tuna miuondombinu kwa maana ya mtandao wa TRA pale, tayari wananchi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wamejenga hilo jengo na tuna rasilimali watu. Sasa nataka kujua ni lini sasa baada ya kutambua kwamba Tarime/Rorya ni Mkoa wa Kipolisi na hivyo ni Makao Makuu ya Mkoa wa Kipolisi, ni lini mtakuja kufunga huo mtambo ili kupunguza adha ya wananchi kwenda kwenye Mkoa wa Polisi wa Mara kutafuta huduma? (Makofi)
Swali la pili ni kuhusiana na kujenga ofisi ya Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya ambao Mheshimiwa Waziri amesema ni mkoa mpya. Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya ni wa siku nyingi ukilinganisha na Katavi, Simiyu na Geita. Kwa mikakati yenu ya ndani ningependa kujua ni lini mtakuja kujenga jengo zuri lenye hadhi ya Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya ili kuondokana na kukaa kwenye magodauni ambayo wanakaa sasa hivi na kushusha hadhi ya Kipolisi Mkoa wa Tarime/Rorya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nirudie majibu yangu ya msingi ambayo nimejibu kwamba, changamoto kubwa ambayo inakabili kutokukamilisha ujenzi wa vituo vya Polisi na miundombinu mingine ikiwemo hii miundombinu ya utoaji wa leseni ni ufinyu wa kibajeti. Azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba mikoa na wilaya zote nchini zinapata huduma hizo muhimu. Changamoto nyingine kubwa ambayo nimeizungumza ni katika mikoa ile mipya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue fursa hii kumhamasisha Mheshimiwa Mbunge, nimefanya ziara katika maeneo mbalimbali ikiwemo hii mikoa mipya na nimeona jitihada mbalimbali ambazo viongozi wa maeneo hayo wamekuwa wakifanya ili kuhamasisha wananchi, pamoja na sisi tupo tayari kuweza kuwasaidia nguvu kazi kupitia Jeshi la Magereza kuanza mchakato wa ujenzi wa vituo vya kisasa kwa mikoa mipya hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati hayo yakiendelea tutaendelea kuhakikisha kwamba tunajitahidi itakavyowezekana kadri ya bajeti itakavyoruhusu kwa upande wetu kujenga vituo hivyo vya Polisi, wakati huo huo kuzungumza na mamlaka ya TRA kuhakikisha kwamba huduma za utoaji leseni zinapatikana katika mikoa na wilaya zote nchini Tanzania, ikiwemo sehemu ambayo Mheshimiwa Mbunge anatoka.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Tarime ina Hospitali ambayo ni Hospitali ya Mji, lakini inahudumia Wilaya nzima, ningetaka kujua ni lini Serikali itajenga Hospitali kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Tarime wakati inasubiria kujenga, iipe ile hadhi kama Hospitali ya Wilaya na kuweza kuleta mahitaji kama inavyotakiwa kwa idadi wa watu wa Tarime nzima na siyo Halmashauri ya Mji tu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kesi anayoizungumzia Mheshimiwa Esther hapa inafanana na ya ndugu yangu Mheshimiwa Chumi, tuna Halmashauri zile za Mji na Halmashauri za Wilaya, kwa bahati mbaya ukiangalia Tarime Halmashauri ya Mji ndiyo ina hospitali, Halmashauri ya Wilaya haina hospitali na bajeti mnayopata ni ndogo, hali kadhalika ukiangalia Mufindi na Mafinga, Mafinga kuna Hospitali ya Wilaya bajeti ikienda inakuwa ndogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimepita maeneo mbalimbali niliwapa maelekezo watu, kwa nini maeneo ambayo hakuna Hospitali ya Wilaya kama kuna hospitali zingine zile za mission tunaweka DDH na tunapeleka funds pale kwa nini kunapokuwa kwa mfano katika Halmashauri ya Tarime kuna Hospitali ya Wilaya, kwa nini watu wa Halmashauri ya Wilaya pale, fedha tunazozipeleka ambao wana bajeti kubwa sana wasielekeze fedha zingine kwa ajili ya kununua dawa na vifaa tiba katika Halmashauri ya Mji.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni jambo nadhani hasa Wakurugenzi wetu katika maeneo husika na viongozi mliopo huko tuangalie haja ya wananchi wetu kuweza kuwahudumia, hili ni jambo kubwa na shirikishi. Kwa hiyo, naomba niagize, katika maeneo ambayo yana scenario kama hii, lazima viongozi mkae muangalie ni jinsi gani tutafanya tuweze kuhudumia eneo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, nakuunga mkono Mheshimiwa Esther Matiko ni jambo lenye mantiki na lina busara zaidi, naomba maagizo haya yachukuliwe sehemu zote kama ni jambo la kujifunza, nini tufanye tuwasaidie wananchi wetu katika suala la afya. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, wakati Naibu Waziri anajibu alielezea ni jinsi gani moshi wa bangi unamuathiri si tu mtumiaji bali hata watu wa pembeni.
Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukiona wakati Serikali inafanya operation ya kukata au kuzuia bangi, inavuna yale mabangi yaliyokwisha komaa, na wanaenda wanachoma zile bangi, sasa Naibu Waziri atueleze ni kwa kiasi gani Jeshi la Polisi wameweza kuathirika na ile bangi na je, hawaoni kwamba zile bangi zinawaathiri ndio maana wanatenda kinyume na wajibu wao wanavyowatakiwa kufanya?(Makofi/ Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwamba kwanza sio jambo la mzaha kuzungumzia masuala yanayohusu dawa za kulevya, kwa sababu zinaathiri vijana wetu, zinaharibu umakini na utimamu wa nguvu kazi ya Taifa letu.
Kwa hiyo, kujibu swali lake sasa ni kwamba wanapoenda kuchoma huwa wanakuwa wamejifunika vifaa maalum na hata kama hawajajifunika vifaa maalum, wakati wanateketeza bangi wakawa passive smoker wa cannabis bado ile bangi ikiingia kwenye mwili wao itakuwa catabolized na kupotea ndani ya miili yao ndani ya siku 30 kwa sababu metabolism ya bangi inadumu ndani ya mwili ndani ya siku 30 baada ya hapo inaisha kabisa inakuwa imekuwa katika form nyingine ya salt inatoka pamoja na mkojo.(Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo hata kama wataathirika lakini madhara yake hayatakuwa ni ya kudumu unless huyo mtu atumie bangi leo, iingie kwenye damu atumie na kesho na kesho kutwa na mwezi ujao awe chronic smoker wa cannabis hapo anaweza akapata madhara. (Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini Waheshimiwa Wabunge ambao wanashughulikia tatizo hili la kupambana na dawa za kulevya wanakumbuka, Mamlaka ya Udhibiti wa Matumizi ya Dawa za Kulevya, mara kadhaa imeenda kwenye kamati hiyo kuelezea matumizi ya sheria na kanuni zilizotungwa chini Ofisi ya Waziri Mkuu, ambazo pia zinaongoza utaratibu mzima wa kuteketeza dawa hizi za kulevya katika maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, unapoona vikosi vile vinafanya
kazi ya uteketezaji wa bangi ziko technics ambazo wanazitumia katika kufanya kazi ya uteketezaji ikiwemo wakati wa uteketezaji pia, wanazingatia uelekeo wa upepo na uelekeo wa hewa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa Wajumbe wa Kamati wanaelewa jambo hilo wanazingatia kwa mfano uelekeo wa upepo na maandalizi mengine ya aina ya matumizi ya vyombo vya uteketezaji ikiwepo aina ya moto utakaotumika katika uteketezaji na aina ya mafuta yatayotumika katika uteketezaji.
Kwa hiyo, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge si kweli kabisa na naomba Bunge lako liondoke hapa likijua kwamba si kweli eti kukitokea tatizo ndani ya Jeshi la Polisi ni kwa sababu wameshiriki katika kuteketeza bangi, na hivyo wameathirika na matumizi ya bangi, ninaomba hilo tuliweke wazi, kikosi kazi kimefundishwa vizuri, polisi wetu ni waadilifu na wanapofanya kazi ile wanafanya kitaalam na kwa kutumia uadilifu mkubwa na kwa kufuata utaratibu.(Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri ametueleza kwamba waliondoa watumishi hewa 19,708. Ni dhahiri kwamba kuondolewa kwa wafanyakazi wenye vyeti fake kumeathiri zaidi maeneo ya elimu na afya. Napenda kujua statistically ni vipi Serikali, maana yake ametuambia wataajiri; mpaka sasa hivi Serikali imeajiri walimu wangapi na wafanyakazi wa sekta ya afya? Maana yake kuna zahanati nyingine hazina kabisa watumishi.
Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine unakuta shule zina walimu watatu tu, tunaweza kuona ni madhara gani watoto wetu watapata. Sasa kama walikuwa na hili zoezi la vyeti fake, walijiandaa vipi ku-replace hawa wafanyakazi kwenye sekta ya elimu na afya? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa kama nilivyoeleza, tumeshatoa vibali hivyo 10,184 na sasa hivi kwa upande wa elimu, tayari Wizara ya Elimu imeanza zoezi la kuchambua, wanatuma vyeti wale ambao walikuwa ni wahitimu na wanaostahiki kuingia, baada ya hapo watahakikiwa na kuweza kuingia katika ajira.
Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika walimu kwa ujumla wake, katika ku-replace watumishi ambao wameondoka kwa walimu, ni zaidi ya walimu 3,012 wataweza kuajiriwa katika zoezi hili. Pia katika suala zima la sekta ya afya, tutaajiri zaidi ya watumishi 3,152. Hili ni katika kuziba pengo la walioghushi vyeti feki. Baada ya hapo, katika mwaka wa fedha 2017/2018 ajira bado ziko pale pale 52,436 na ni kutokana na hali ya uwezo wa kibajeti.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ni kweli kabisa kwamba wastaafu wanateseka sana na wengi wao wanapoteza maisha. Ni katika Bunge hili hili, Mheshimiwa Naibu Waziri aliliahidi Bunge kwamba wastaafu wote wanaodai malimbikizo baada ya marekebisho ya kima cha chini kutoka shilingi 50,000 kwenda shilingi 100,000 watalipwa fedha zao kwa maana arrears zote lakini ni takribani miaka miwili sasa wastaafu hawa hawajalipwa fedha zao sana sana ni wale ambao walikuwa kwenye PSPF na PPF.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningetaka kujua ni kwa nini Serikali haijaweza kuwalipa hawa wastaafu haya malimbikizo kama ambavyo Naibu Waziri uliahidi Bunge hili na je mnavyoenda kuwalipa…
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kukanusha kwamba ni miaka miwili wastaafu hawa hawajalipwa ile nyongeza, siyo sahihi hata kidogo. Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii wameanza kulipa kima cha chini kilichoongezwa na Serikali kuanzia mwezi Januari, 2017. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili aliloli-quote yeye kwamba niliahidi hapa, nakumbuka wakati najibu swali hili nililieleza Bunge lako Tukufu kwamba kulingana na Sheria ya SSRA, regulator anaye-regulate Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii, ni Bodi za Wadhamini za mifuko husika baada ya actuarial valuation ndizo zinazoamua sasa kulipa kiwango hiki na ndipo baada ya kufanya actuarial valuation Bodi zote zimeidhinisha na tumeanza kulipa kwa kipindi chote kuanzia Januari mpaka leo tunapoongea wote wanalipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua yapo malalamiko wanasema kwamba wengine hawaoni hizo transaction lakini naomba niwaambie kwamba hasa kwa wastaafu wetu wanaolipwa na PSPF siku za nyuma pensheni zao za kila mwezi zilikuwa zikianza kulipwa kabla ya hii addition kwa hiyo kulikuwa kunaonekana kuna two transaction ndani ya mwezi mmoja kwa utofauti wa wiki moja au wiki mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali yetu inalipa nyongeza hii kwa sababu nyongeza hii hasa kwa PSPF hulipwa kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, tunalipa kwa wakati na wanalipwa siku moja pensheni yao pamoja na ile nyongeza yao. Kwa hiyo, hakuna sehemu yoyote ambapo hawalipwi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kufuatia majibu ya Mheshimiwa Waziri, ni dhahiri kabisa imeonyesha ni jinsi gani miundombinu ya kujifunzia na kujifunza katika Halmashauri ya Mji wa Tarime hairidhishi na inapelekea matokeo mabaya kwa ufaulu wa wanafunzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wa Tarime wameitikia sana wakishirikiana na wadau mbalimbali ikiwepo mimi mwenyewe Mbunge. Tumejenga madarasa mengi lakini mengi yamekaa bila kuezekwa na kwa kuwa kuna Shule ya Msingi Mtulu ambayo imejengwa na wananchi kwa kujitolea madarasa sita pamoja na ofisi lakini Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji amezuia ile shule wananchi wasiendelee kujenga kwa kile anachokiita kwamba ni mgogoro wa ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sasa kupitia Wizara hii ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais na Rais ana mamlaka ya kubadilisha matumizi ya ardhi, wawatie moyo wananchi wale waliojenga yale madarasa ili sasa waweze kuamuru ile shule iendelezwe ili kupunguza adha ya upungufu wa madarasa katika Halmashauri ya Mji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Halmashauri ya Mji kuna shule moja ambayo inatumiwa na shule tatu, Shule za Msingi Azimio, Mapinduzi na Sabasaba. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kipindi hicho akiwa Naibu Waziri alitembelea sisi kama Halmashauri ya Mji tunataka ile shule ijengwe ghorofa ili sasa walimu wasikae kwenye mti kama Ofisi, wanafunzi wasifundishiwe nje chini ya mti, wanafunzi wasirundikane 120 kwenye darasa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini sasa Serikali isiweze kutumia ile asilimia tano ambayo walisema Waziri anaweza akapeleka kwenye matumizi mbalimbali kama tulivyoona ilivyoenda Chato kwenye uwanja wa ndege. Kwa nini msijenge ghorofa katika shule ile kwenye zile asilimia tano ambazo ni zaidi ya shilingi trilioni 1.7 ili sasa kupunguza adha ya ukosefu wa madarasa katika Mji wa Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema ukisikia upande mmoja, hakika upande ambao haujasikilizwa utakuwa lazima umekosa. Itakuwa ni vizuri tukajiridhisha sababu ambazo zimesababisha Mkurugenzi azuie uendelezaji wa hiyo shule ili tunapokuja kutoa taarifa iwe ni taarifa ambayo iko balanced. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie mbunge, miongoni mwa maeneo ambayo nitatembelea ni pamoja na kwenda kutazama uhalisia wa hiki ambacho nakisema kwa sababu lengo ni kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano wa vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaase Waheshimiwa Wabunge na viongozi kwa ujumla, kwamba katika Wilaya ya Tarime, vijana ambao wanamaliza kuanzia darasa la kwanza mpaka darasa la saba wapo 25,000 lakini vijana ambao wanajiandaa kuingia darasa la kwanza wapo 13,000; kwa hiyo, unaweza ukaona sisi kama taifa kuna mambo ambayo lazima tu-address namna ya population growth inavyokwenda, tukiacha tukatizama hivi tukidhani kwamba Serikali peke yake inaweza hakika haiwezekani. Ni vizuri tukashirikishana pande zote ili kutatua matatizo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya swali lake la pili juu ya ujenzi wa ghorofa, ghorofa jambo zuri na ningependa na mimi nijiridhishe halafu tuone na uwezo wetu maana unapotengeneza chakula lazima ujue na unga upo kiasi gani kwa sisi tunaokula ugali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na juu ya asilimia tano nitaomba niwasiliane na Mheshimiwa Mbunge tuone hiyo asilimia tano na tutayamaliza ili tatizo hili liweze kutatuliwa lakini siamini kwamba asilimia tano inajenga ghorofa. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mkoa wa Mara una shughuli nyingi sana ambazo zingeweza kuliongezea Taifa letu uchumi kwa maana ya utalii, tuna Ziwa Victoria lakini pia makumbusho ya Baba wa Taifa. Katika majibu yake Naibu Waziri ametueleza kwamba wamefanya usanifu pia kwenye uwanja wa ndege wa Musoma, ningependa kujua uwanja wa ndege wa Musoma na wenyewe upo kati ya viwanja vilivyopewa priority maana yake umetaja Tanga tu kama ndiyo umepewa kipaumbele na unaanza kukarabatiwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Kwenye jibu langu la msingi wakati najibu kuhusu uwanja wa ndege wa Tanga nilieleza viwanja 11 ambavyo vimeshafanyiwa Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na uwanja wa Musoma ukiwemo. Ni kweli kwamba viwanja vyote vimepewa kipaumbele kinacholingana na pesa itakapopatikana kama nilivyoeleza tutafuta mkopo kutoka Benki ya Dunia, pesa itakapopatikana basi viwanja vyote vitapewa kipaumbele kujengwa kwa sababu tunahitaji viwanka vyote vya Mikao viwe na kiwango kizuri ambacho ndege yoyote inaweza ikashuka, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, napenda kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa magereza mengi nchini ni kweli miundombinu ni michakavu sana; na kwa kuwa asilimia zaidi ya 75 mahabusu waliopo magereza ni wale ambao wana kesi za kudhaminika lakini wananyimwa dhamana. Swali langu linakuja kwamba Gereza la Tarime linachukua mahabusu na wafungwa kutoka Wilaya ya Rorya na unakuta ina msongamano mkubwa kutoka 209 mpaka 560 mpaka 600.
Mheshimiwa Spika, ningependa kujua sasa Serikali ni lini itajenga gereza Rorya, kwa sababu ile ni Wilaya inajitegemea, ili kupunguza msongamano wa mahabusu na wafungwa Tarime ambayo inaweza ikapelekea magonjwa mbalimbali na ukizingatia miundombinu ni mibovu sana? Lakini pia kwa haki za kibinadamu wanatoka kule Rorya kufuatilia kesi Tarime, kuja kuona mahabusu Tarime, kuja kuona wafungwa Tarime. Ni lini sasa mtajenga Gereza la Rorya kupunguza msongamano katika Gereza la Tarime? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tunakiri kwamba kuna msongamano wa wafungwa katika Gereza la Rorya na kuna umuhimu mkubwa wa kujenga Gereza pale. Lakini changamoto ya upungufu wa magereza katika Wilaya zetu mbalimbali nchini halipo Rorya tu; kwenye maeneo mengi ya Wilaya nchini bado magereza yamekuwa ni upungufu.
Kwa hiyo tutajaribu kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano huo kwa kujenga magereza katika Wilaya ambazo zina upungufu katika nchi nzima, na utekelezaji wa mpango huo utategemea upatikanaji wa rasilimali fedha, kwani mpaka sasa hivi kati ya Wilaya 92 ni Wilaya 43 nchini ndio ambazo zina magereza.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kimsingi tunalifahamu hili tatizo, niombe tu Mheshimiwa Mbunge awe na subira pale ambapo hali itakapo ruhusu tutashughulikia pamoja na hizo Wilaya nyingine 43 ambazo nimezizungumza zenye mapungufu hayo. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kiukweli majibu ya Mheshimiwa Waziri yapo kiujumla zaidi na inasikitisha kwa sababu tunapokuwa tunatoa maswali yetu tunatarajia mwende sehemu husika kujua uhalisia wa sehemu husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mahabusu waliopo Gereza la Tarime, zaidi ya asilimia 65 ni kesi au makosa ambayo yanatakiwa yapewe dhamana; na kwa kuwa kesi nyingi ni kesi za kisiasa za kubambikwa na nyingine ni kesi za watoto chini ya miaka 15; na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri alikuja Tarime na hakupata muda wa kuingia Gerezani, ningependa sasa leo mtuambie ni lini Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Katiba na Sheria, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mkurugenzi wa Mashtaka watakuja Tarime kuangalia hali halisi ya mahabusu walioko Gereza la Tarime ili waweze kuondoa zile kesi ambazo jana Mheshimiwa Waziri alikiri kwamba nyingine ni za juice, ili Watanzania warudi uraiani na wafanye kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kuna msongamano mkubwa sana kwenye Gereza la Tarime, capacity yake ilikuwa ni watu 260 wakiwa wamezidi sana. Sasa hivi ni zaidi ya watu 600; na kwa kuwa ukitokea mlipuko wa magonjwa tutapoteza Watanzania wengi waliopo kwenye lile Gereza; na kwa kuwa gereza lile linahudumia Wilaya ya Rorya na Tarime: ni lini sasa Serikali ya Chama cha Mapinduzi mtajenga gereza katika Wilaya ya Rorya, mtajenga Mahakama ya Wilaya kule Rorya ili wale Watanzania wa Rorya waweze kushtakiwa kule na kuhudhuria kesi zao kule ili kuondoa msongamano ambao upo katika Gereza la Tarime?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwape pole timu yangu ya Magereza (Tanzania Prisons) kwa kushindwa jana kwa figisu za Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda zilipocheza na Ndanda. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wizara ya Mambo ya Ndani, Mwanasheria Mkuu na Wizara ya Katiba na Sheria tutalifanyia kazi jambo hilo; huo ni wajibu wetu na tumekuwa tukifanya hivyo. Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria ameshafika Mkoa wa Geita, ameshafika Mkoa wa Mwanza, Mkoa wa Kagera na anakuwa na Ofisi ya DPP na anakuwa pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani. Nikubaliane nalo, hilo tutafanya, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba wale ambao kwa kweli wanaweza wakapata namna ya kwenda nje waende nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitofautiane na Mheshimiwa Mbunge kwenye takwimu, anasema asilimia 75 ya kesi ni za Wanasiasa. Natofautiana naye kwa sababu amesema asilimia 75 ni za wanasiasa na wakati ule ule ni za watoto. Huwezi ukawa na asilimia 75 ya wanasiasa na watoto. Kwa hiyo, kwenye hilo siyo kweli na kama kuna issue specific ya kesi ya mtu mmoja mmoja, Waheshimiwa Wabunge ninyi ni Viongozi, tusaidiane kupeana taarifa ili tuweze kufanya intervention inayostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kujenga gereza Rorya hata Mheshimiwa Mbunge wa Rorya amelisema mara nyingi na ameongelea matatizo wanayopata wananchi wake. Ni kweli wanapata shida kwa sababu mashahidi wanatakiwa kutoka Rorya na ni gharama hata kwa Serikali kuwatoa watu Wilaya nyingine kwenda kutoa ushahidi katika Wilaya nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo tumelipokea na kama Serikali tunachukua hatua kwa Wilaya zote mpya ambazo zimeanzishwa, ambazo bado hazina huduma hizo za Mahakama pamoja na Magereza, kuhakikisha kwamba tunawapunguzia usumbufu wananchi na sheria iweze kuchukua mkondo wake kwa wakati.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Chuo Cha Maendeleo ya Wananchi Tarime miundombinu yake ni mibovu sana na haina hadhi ya kuwa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi. Kwa bajeti ya mwaka jana 2016/2017, Serikali iliahidi hapa kwamba Vyuo vyote vya Wananchi vitapandishwa hadhi na kuwa VETA. Napenda kujua sasa ni lini Serikali itaenda kutimiza azma yake ya kupandisha Vyuo hivi vya Wananchi kuwa VETA kwa kuanzia na Chuo cha Wananchi cha Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kuna dhana ya kufikiria kwamba labda mafunzo yanayotolewa na VETA ni bora zaidi kuliko yale yanayotolewa na Chuo cha Wananchi. Nitake tu kusema kwamba Vyuo vya Wananchi vina uwezo mzuri na mkubwa sana katika kutoa mafunzo isipokuwa kwa muda mrefu vilikuwa havijapewa haki yake ya kuendelezwa na kufanyiwa ukarabati unaostahili pamoja na kuwekewa miundombinu na vitendea kazi vya kufundishia kama inavyostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu Wizara imetenga jumla ya shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kufuatilia vyuo hivyo na kuvirekebisha. Kwa hali hiyo, tutafuatilia pia Chuo cha Tarime kama alivyoeleza Mheshimiwa Mbunge ili kiweze kusaidiwa.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ingawa kwa kweli majibu ya Waziri, Naibu Waziri yanakatisha tamaa maana tumekuwa tukisikia siku zote kadri fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ulinzi wa raia na mali zao ni muhimu sana katika nchi yetu. Kwenye Jimbo la Tarime Mjini katika Kata zote nane tuna kituo cha poilisi kwenye Kata ya Bomani tu, na Kata zingine ambazo za pembezoni wananchi wamejitolea kujenga vituo vya polisi. Tunataka kujua mkakati thabiti wa Serikali katika ku-support zile juhudi za wananchi hasa Kata ya Nyandoto, Kenyamanyoli, Nkende na Kitale ambazo ni mbali na mji, na kuna gari moja tu ambayo inafanya patrol.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nini mkakati wa Serikali maanake mnakusanya mapato mengi, muweze kuelekeza kwenye kumalizia vituo vya poilisi ili tuweze kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nieleze tu kwa ufupi, ni kwamba changamoto ya vituo vya polisi haipo tu katika vituo vya polisi vya ngazi ya kata na tarafa, tuna Mikoa ya kipolisi takribani 34 nchi nzima. Kati ya hiyo majengo ambayo ya makamanda wa mikoa yaliyopo nchini ni 19. Kwa hiyo takribani mikoa 15 haina Ofisi ya Makamanda wa Mikoa. Mikoa miwili Manyara na Mara ndiyo ambapo ujenzi wa Ofisi mpya za makanda unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mtaona changamoto hii ni pana sana, na ndiyo maana wakati wote tumeendelea kuwashawishi wadau werevu ikiwemo ninyi Waheshimiwa Wabunge ambao wengi wenu mmekuwa mkijitolewa na sisi tumekuwa tukichukua jitihada mbalimbali kuhamasisha wananchi kujitolea kuchangia ujenzi wa vituo hivyo vya polisi ili kabiliana na changamoto hii; wakati ambapo Serikali kila mwaka imekuwa ikitenga bajeti kwa ajili ya ujenzi pamoja na ukarabati wa vituo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii haiwezi kumalizika kwa wakati mmoja. Naamini wewe Mheshimiwa Mbunge ni Mbunge wa Jimbo na una fedha za Mfuko wa Jimbo. Unaweza ukatumia hizo vilevile kusaidia jitihada hizi za Serikali katika kuhakikisha kwamba ina punguza changamoto ya upungufu wa vituo vya polisi nchi nzima kuanzia ngazi ya Wilaya, Kata na Tarafa. Serikali kama ambavyo tunasema pale fedha zitakapopatikana tutapunguza tatizo hili hatua kwa hatua, hatuwezi tukamaliza kwa wakati mmoja.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nashukuru kwamba, Wizara inatambua kwamba Mji wa Tarime unatakiwa kupimwa, lakini pia inatambua kwamba una upungufu wa watumishi. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa maeneo mengi ya Mji wa Tarime yalikwishaandaliwa ramani ya Mipango Miji, lakini mpaka sasa hivi hayajapimwa, na kwa kuwa wananchi wanaendelea kujenga kiholela na kuharibu ramani ambayo tulikwishaandaa hapo awali, ni kwa nini sasa Serikali msiweze kuunda kikosi kazi kwa ajili tu ya kuja kupima maeneo yote ambayo yameshaandaliwa ramani ya mipango miji ili sasa tusiharibu hii ramani ambayo imeshaandaliwa?
Swali la pili, kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Tarime haina vifaa vya kuweza kupima ardhi na tumekuwa tukikodi kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Musoma, na kwa kuwa, Halmashauri ya Mji wa Tarime hatuna fedha za kuweza kununua vifaa hivi ambavyo vinauzwa bei ghali sana, ni kwa nini sasa Serikali isiweze kufadhili ununuzi wa vifaa hivi ili kuweza kupima maeneo mengi zaidi na kuweza kuharakisha umilikishaji wa ardhi kwa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anasema maeneo mengi ya Tarime yalikuwa yamepimwa, yana michoro tayari, lakini upimaji wake pengine haujakamilika na yameanza kuvamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali hilo naomba nijibu kwamba kwanza niwaombe Halmashauri yenyewe husika kwa sababu ndio kwanza inazidi kukua sasa hivi, kama maeneo yale hayajakamilika katika upimaji niombe Halmashauri iwe makini katika kulinda yale maeneo yasivamiwe, kwa sababu katika maeneo yote yenye michoro wananchi wanapovamia, hapatakuwa na upimaji mpya. Maana yake wakikutwa wamevamia kiwanja kimoja watu wawili/watatu, maana yake pale lazima mmoja itabidi apishe apewe kile kiwanja na mwingine atafutiwe eneo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufanya lile eneo lisiingiliwe na watu wengi zaidi niwaombe sana Halmashauri kwanza wakamilishe ile taratibu kwa sababu ni jukumu pia la Halmashauri, lakini watasaidiwa pia na Ofisi yetu ya Kanda ambayo sasa hivi wamesogezewa, itakuwa iko Simiyu. Kwa hiyo, tukishafanya hivyo tutakuwa tumelinda yale maeneo. Urasimishaji unaofanyika hauwezi kufanyika katika yale maeneo ambayo tayari yalikuwa yamepimwa, unafanyika katika maeneo ambayo yapo katika ule utaratibu upo.
Kwa hiyo, suala la kuwa na vikosi kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, kazi hii inafanyika haraka ni jukumu pia la Kanda husika kwa sababu, tunaweza tukatumia Wataalam walioko katika Halmashauri jirani wakiratibiwa na Ofisi ya Kanda, suala hilo linaweza likafanyika na inawezekana kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la vifaa; suala hili nilishalijibu pia katika majibu ya nyuma katika Bunge hili. Niombe sana Wizara haiwezi kununua vifaa vya upimaji katika Halmashauri zote, ni jukumu la kila Halmashauri kuweka bajeti zake, Wizara imejipanga katika Kanda zake na vifaa vile katika Kanda vinaweza kutumika katika Halmashauri yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi vifaa vile vina bei kubwa sana, lakini ninaomba na nimekuwa nikielekeza wale wenzetu walioko kwenye Kanda, kila mmoja ana Halmashauri zake ni kiasi cha kupanga utaratibu mzuri, mkiwa na vikosi kazi ambavyo vinaweza vikasaidia katika kwenda Halmashauri moja baada ya nyingine itaturahisishia katika kupunguza kero ya upimaji.
Kwa hiyo, naomba pamoja na private sector ambao wanatumika, bado Ofisi zetu za Kanda kwa kutumia watumishi katika Halmashauri kwenye Mkoa husika tunaweza tukapunguza tatizo hilo. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ningependa Serikali ituambie kwa muktadha wake kabisa kwa sababu haya ambayo wameelezea kuyafanya it is a peanut! Ni madogo sana. Kujenga kituo cha Makumbusho, kuwafadhili watu kupata fani ya malikale ni hela ndogo sana! Mjusi huyu tangu apelekwe kule ni kiasi gani, kwa maana ya faida kutokana na utalii, umeiingizia Serikali ya Ujerumani? Kwa nini Serikali ya Tanzania tusiingie angalau mkataba tuwaambie angalau asilimia tano au 10 ya mapato watuletee kutokana na mjusi ambaye anaingiza fedha za utalii kule Ujerumani kuliko hizi peanut package ambazo wanatupa ambazo hazisaidii nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshauri tu Dada yangu kwamba, masuala yanayohitaji utafiti na takwimu ni vizuri kusubiri utafiti na takwimu utoe matokeo badala ya kutoa kauli za jumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda niseme tu kwa kifupi kwamba, mjusi huyu au mijusi hawa waliotoka Tanzania kule Ujerumani na bahati nzuri wako baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa wamefika pale mahali na mmojawapo ni Mheshimiwa Dkt. Kafumu ni kwamba, mijusi hawa wawili ni sehemu tu moja ya vivutio vingine vya malikale vilivyoko katika jumba la makumbusho kule Ujerumani ambalo ni kubwa na lina vitu vingi na kiasi ambacho hata kukokotoa kwamba, mijusi wawili wa Tanzania wanazalisha nini ndani ya jumba ambalo watu wanakuja kuangalia vitu vingi ambavyo Wajerumani hawa walivitoa katika nchi za Afrika walizotawala wakati huo katika maeneo mengi na wako wengi kwa kiasi hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mambo matatu ambayo yanafahamika tayari ni kwamba, viingilio katika makumbusho ya Elimu Viumbe huko Berlin ni Euro 3.5 hadi Euro nane, kwa jumba zima ambalo lina vivutio vingi ambapo wanafunzi, watafiti na wazee wanaingia bure, hilo la kwanza.
Pili, asilimia 95 ya Bajeti ya Makumbusho ya Elimu Viumbe Berlin kule, inatoka katika Serikali Kuu na Serikali ya Mji wa Berlin, maana yake ni kwamba, hiyo makumbusho haina hata uwezo wa kuweza kujiendesha yenyewe.
Tatu, Makumbusho ya Elimu Viumbe ya Berlin ina kumbi nyingi za maonesho, Ukumbi wa Dinosauria ukiwa ni mmoja tu, kwa hiyo, ni vigumu kujua kiasi halisi cha fedha kinachopatikana kutokana na kuingia na kuona masalia ya mijusi wa Tanzania. Vilevile kwenye makumbusho hii kuna nakala ya masalia ya mijusi kutoka nchi nyingine duniani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunapozungumzia suala la kuboresha eneo hili ambako mijusi wametoka, ili liweze kuwa eneo la utalii si sahihi kusema kwamba, kipato kitakachotoka pale kitakuwa peanut. Pia, pili, ukifundisha watu kwenye taaluma hiyo ya malikale ambayo itaendelea kufanya tafiti katika nchi nzima hii, athari yake ni kubwa. Kwa hiyo, kiufupi unaweza kusema tu kwamba, watu hawa sasa badala ya kutupa samaki wanataka kutupa boti, wanataka kutufundisha kuvua, ili tuweze kuvua wenyewe samaki tupate faida zaidi kuliko kupewa samaki wa siku moja tu. (Makofi
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu alitueleza kwamba kuna Madawati ya Jinsia 117. Hii inaonesha dhahiri kwamba kuna Wilaya nyingine hazina haya Madawati ya Jinsia. Ni ukweli kabisa kwamba kiwango cha ubakaji kwa maana ya watoto wa kike lakini na ulawiti wa watoto wa kiume kimekuwa kikiongezeka sana na tunajua sheria zipo. Ni kwa nini hawa watu wanaendelea kufanya hivi labda ni kutokana na mianya ambayo ipo kuanzia kwenye Jeshi la Polisi na kwingineko.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua kwa sababu sheria zipo lakini bado vitendo hivi vinaendelea, ni kwa nini sasa Serikali isije na njia mbadala kama tiba kabla ya hili tukio kutokea, kuwafanyia kama counseling hao wanaotenda kwa maana kwenye maeneo husika wazazi au jamii husika ili tuwe na tiba mbadala kabla ya tukio kutokea kwa sababu tunaona haya mambo yanatokea na sheria zipo ni kwa nini msibuni …
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali inafanya njia mbadala nyingi tu na niweke tu kumbukumbu sawa kwamba Madawati ni zaidi ya 417 na kwenye Vituo vya Polisi vyote tumeweka Madawati ya aina hiyo ili kuongeza idadi iwe kubwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu njia mbadala, kama Serikali tumeendelea kuongeza jitihada za kutoa elimu licha ya hatua kali tunazozichukua. Ndiyo maana tunaendelea kuwasihi hata viongozi wa kiroho kwenye nyumba za ibada kuendelea kutoa elimu hiyo kwa sababu matukio haya maeneo mengi yanaambatana na imani za kishirikina. Wengine wanaamini wakifanya hivi watapata utajiri, wengine wanakuwa na kesi wanaamini wakifanya hivyo watakuwa wamesafishika kwenye kesi hizo na wengine wanaamini watapona magonjwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, jamii kwa ujumla wake katika maeneo tofauti tofauti tumeona tupanue elimu hasa hasa zikiwepo nyumba hizo za ibada kwa sababu maeneo ambapo nyumba za ibada watu wameshika sana mienendo ya Kimungu matukio haya ya kikatili yamekuwa pungufu zaidi. Kule ambapo kuna imani nyingi za kishirikina ndiko ambapo matukio haya ya ajabu ajabu yamekuwa yakiendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya kazi hiyo kuwapa viongozi wa kiimani tunaendelea kutoa rai kwa wananchi kutoa taarifa ili sisi kwa upande wa Serikali tuweze kuchukua hatua kali kwa wale watakaobainika wamefanya hivyo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli kabisa kwamba msongamano kwenye Magereza yetu Tanzania, Tarime na hata Segerea nilipoenda ni mkubwa sana.
Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza ambalo nauliza hapa, Mheshimiwa Waziri wakati anatoa takwimu za gharama kwa wafungwa, amesema ni shilingi 1,200 kwa chakula. Nilipokuwa Segerea kwenye swali langu ninaloenda kuuliza, kule kuna wamama wamefungwa wanadaiwa shilingi 150,000 mathalani, lakini amefungwa miezi sita. Kwa gharama ambazo amezitoa Mheshimiwa Naibu Waziri unakuta zinavuka pale tena mpaka shilingi 270,000. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna mama ambaye amefungwa miezi sita, anaumwa ugonjwa wa fibroid ana-over breed, kila siku jioni ambulance inampeleka Amana.
Je, ni kwa nini Serikali isitumie busara ya zaidi kwa hawa akina mama ambao wengine wana watoto wachanga ambao unakuta wanafungwa kwa kesi za shilingi 100,000 au 200,000 wasiweze kuzi-waive uki-compare na gharama ambazo wanaenda kuhudumia kwenye ile jamii? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, suala la kwamba fedha ambayo wanadaiwa ni kidogo, ni suala la kisheria. Kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge anafikiri sheria ile imepitwa na wakati na haitendi haki, ni rahisi yeye kuleta hoja Bunge hili libadilishe sheria kwa sababu sheria ndiyo zinasema hivyo. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nipongeze kwa majibu mazuri yaliyotolewa. Nataka tu kumuomba Mheshimiwa Mwalongo kwa ile hoja ya jambo mahususi alilolileta kwamba baada ya Bunge, basi tuonane ili nilipate vizuri kwa sababu jambo lake alilolileta lile ni mahususi ili tuweze kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambazo tumezipata, niweke tu kumbukumbu sawa, siyo kila Magereza yana msongamano. Tuna baadhi ya Magereza ambako katika mikoa ile kiwango cha uhalifu ni kidogo, hata msongamano Magerezani ni mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilienda Mkoa wa Lindi, Gereza lilikuwa na uwezo mkubwa kuliko kiwango cha wahalifu. Hivyo hivyo, nilienda kwa Mheshimiwa Shangazi kule, kiwango cha Gereza la kule ni kikubwa kuliko wahalifu walioko mle.
Kwa hiyo, nitoe rai kwa Watanzania na jamii nzima ya Watanzania kuepuka kufanya uhalifu kwa kweli, kwa sababu sisi kama Serikali hatupendi watu kuwa magerezani, lakini tunawapeleka kwa sababu ya uhalifu wanaoufanya.
Mheshimiwa Spika, hatuwezi tukaacha wahalifu wakawa nje na kama watu watafanya uhalifu, ni kwamba wataenda magerezani. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa nioneshe masikitiko yangu na kwa namna gani Serikali haiwezi kuweka kumbukumbu. Mwaka 2016 niliuliza swali hili na majibu walinipa haya haya licha ya kwamba aliyekuwa Waziri alikuja Tarime na akajionea hali halisi na akatoa agizo kwamba ule mnada ufunguliwe, lakini leo mnaleta majibu ya kumbukumbu za mwaka 1997. Maswali yangu mawili ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wafanyabiashara wa ng’ombe wanapeleka ng’ombe nchini Kenya kwa mnada ambao upo mpakani wa Mabera kupelekea upotevu mkubwa wa mapato ambayo yangekuja Tanzania kupitia multiplier effect, Wakenya wangekuja kununua zile ng’ombe Tanzania kwa sababu wanategemea ng’ombe za kutoka Tanzania kuliko ilivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Spika, ni kwa nini Serikali hamkutaka kutumia rejea ya muhtasari ya kikao cha mwaka 2016 ambapo tulikaa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Tarime, Waziri na watendaji wa Wizara husika pamoja na mimi Mbunge na baadaye tukaongea na wananchi? Kwa nini hamkutumia ule muhtasari ili mweze kufuata maamuzi yaliyofikiwa kuweza kufungua Mnada wa Magena?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wafanyabiashara wa ng’ombe ambao wanapeleka Kenya wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa sana kwenye kuvusha ng’ombe hizi. Kwa kuwa mnada ambao wameuweka rejea wa check point ya Kirumi hautoi suluhishi, kwa sababu wakinunua ule mnada siyo wa mpakani wanapokuja kuvusha ng’ombe kwenda Kenya wanasumbuliwa sana.
Ni kwa nini sasa Waziri (maana yake inaonekana hamtunzi kumbukumbu) husika usije tena kwenye Mnada wa Magena uweze kujionea uhalisia na maamuzi yale ili sasa uweze kuruhusu mnada huu kufunguliwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko na kwa hakika Mheshimiwa Esther Matiko anashiriki kikamilifu katika kumuunga mkono Mheshimiwa Rais juu ya ulinzi wa rasilimali za nchi yetu na ndiyo maana anasisitiza sana kuhakikisha rasilimali za mifugo zinaweza kudhibitiwa pale ili ziweze kuinufaisha nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza anatusisitiza kwa nini tusitumie Mnada wa Magena sawa na muhtasari wa mwaka 2016 ilipokaa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya kule
Mara na Wizara yetu; na swali la pili, kwa nini Mheshimiwa Waziri asiende Magena?
Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie kwamba hivi sasa Wizara yetu imeunda tume maalum ambayo inapitia maeneo yote katika nchi yetu kufanya tathmini ya minada tuliyonayo ya awali zaidi ya 480 na minada ya upili na mipakani ili kuweza kujiridhisha na maombi yaliyoletwa. Nataka nimwambie kwamba moja ya eneo ambalo tutalifanyia kazi baada ya tathmini hii inayokwenda kukamilishwa na Wizara na wataalam wetu, ni hili alilolileta hapa Mheshimiwa Esther Matiko.
Mheshimiwa Spika, kwa kumhakikishia ni kwamba tutafika Magena pia. Mimi kama Naibu Waziri na Waziri wangu tutakubaliana, tutakwenda Magena kujiridhisha na hiki anachokisema. Kwa faida ya nchi yetu, tukiona kwamba jambo hili lina faida nasi, tutalitekeleza sawa na ushauri wake. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Spika, Jimbo la Tarime Mjini, Kata za Nkende, Kenyemanyori, Kitare, Nyamisangura na Turwa pamoja na Nyandoto hazina umeme kabisa, Bunge lililopita niliuliza swali kama hili na Naibu Waziri akaahidi atatembelea Tarime ili kuweza kuona wakandarasi wa REA ambao tangu mwaka 2016 walitakiwa watekeleze huu mradi, lakini mpaka leo ni Kata ya Nyandoto ndiyo tumeona sasa wameanza kufanyakazi.
Je, ni kwa nini Naibu Waziri hukuweza kutekeleza ile ahadi ambayo uliahidi kwa wana Tarime ili waweze kupata huu umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru kwa kutambua kwamba kazi imeanza ka Kata ya Nyandoto kama alivyoitaja, naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kuwa ahadi yangu ya kutembelea Jimbo la Tarime Mjini na Mkoa wa Mara iko pale pale ila kutokana tu muingiliano wa ratiba, lakini kwa kuwa kazi zetu ziko site naomba nimthibitishie baada ya Bunge hili nitatembelea Wilaya hiyo ya Tarime na Wilaya zingine za Mkoa wa Mara kuhamasisha na kukagua miradi hii na kuwapa shime wakandarasi wafanyekazi kwa haraka na kama inavyokusudiwa. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hili swali la kuuliza kuhusu uwanja wa ndege na kuiomba Serikali ione umuhimu wa kuupandisha hadhi huu uwanja utoke kwenye Halmashauri na uende kwenye Tanzania Aviation Authority; kwa sababu kwa sasa hivi ilivyo kumkodisha Coastal Aviation kwa milioni 20 kwa mwaka anakuwa ana-monopolize na kodi ambazo anawataja aviation zingine wanavokuja kutoa pale ni nyingi sana; kwa hiyo Serikali tunapoteza mapato mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali, ni kwa nini sasa Serikali haioni umuhimu wa kupandisha hadhi huu uwanja na kuukarabati kwa sababu tunapata watalii kutoka maeneo mbalimbali, lakini pia unaweza kutumika kwa ndege kutoka pale kwenda hata nchi jirani ya Kenya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kwa nini sasa wameeleza hapa kwamba wamekarabati barabara ya kilometa 1.2, lakini kuna barabara ya kutoka Tarime kupita Magena unaenda mpaka Kata ya Mwema kule ambapo kuna daraja la Mto Moli ni bovu sana hata Clouds Tv walionesha…..
…linahatarisha maisha watu wanaotumia ile barabara. Ni lini sasa Serikali itaweza kujenga daraja lile la Mtomoli sambamba na ile barabara ambayo inaenda Magena kwenye huu uwanja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya kuomba kupandishwa uwanja huu kuchukuliwa na iwe miongoni mwa viwanja ambavyo vinamilikiwa kitaifa haina ubaya. Hata hivyo ni vizuri tukajua chimbuko la uwanja huu. Uwanja huu mwanzo ulikuwa unatumiwa na kampuni hii ambayo inajiita COGFA ambao wanajenga barabara ya kutoka Sirari kwenda Makutano. Na wao baada ya kumaliza matumizi yake walimkabidhi Mkuu wa Wilaya, lakini baadae bali katika kugawanyika Halmashauri ya Mji na halmashauri ya Tarime Town Council na DC ikaonekana kwamba uwanja ule ambao uko kilometa tisa ubaki chini ya umiliki. Ukitazama katika mkataba wao ambao ni suala la wao ndani ya Halmashauri, kwa sababu mkataba umeingiwa kati ya Coastal Aviation na Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo linaongeleka, kwa kadri watakavyopisha kwenye vikao vyao na wakaridhia kwamba sasa ownership ihame sisi kama Serikali hatuna ubishi na hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya swali la pili la kujenga daraja, kama ambavo tumekuwa tukitengeneza miundombinu kwa kadri bajeti inavyoruhusu, naomba nimehakikishie Mbunge bajeti ikiruhusu tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba mazingira rafiki kwa ajili ya watalii kwenda mbuga yanajenga, ni pamoja na kujenga kwa daraja.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Soko la Kimataifa la Lemagwi ambalo lilikuwa limejengwa na baadaye kutelekezwa, liko Wilayani Tarime, ambalo lingeweza kusaidia kuuza mazao mbalimbali. Tungependa kujua, ni lini Serikali itamaliza kujenga hilo soko ambalo limetumia zaidi ya billions za Watanzania na baadae limetelekezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali wka kuzitaka halmashauri zote ambazo zina miradi ya kimkakati ambazo wana uhakika katika uwekezaji pesa inakwenda kupatikana ikiwa ni pamoja na Halmashauri ya kwao, ni vizuri wakahakikisha kwamba andiko linakamilika ili kama kuna sehemu ambayo Serikali inahitaji kuwekeza nguvu yake tujue exactly nini ambacho tunakwenda kukipata kama halmashauri kabla ya nguvu kubwa haijawekezwa huko.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amejibu kwamba ikigundulika askari wanaowaweka kituoni wananchi kwa muda watachukuliwa hatua. Wakati nachangia bajeti iliyopita ya Wizara ya Mambo ya Ndani nilieleza bayana kabisa kwamba kuna baadhi ya mahabusu kituo cha Kawe waliwekwa ndani kwa zaidi ya miezi mitatu na nikasema kabisa na nikamtaja na askari aliyehusika mpaka leo hajachukuliwa hatua.
Je, ni kwa nini Mawaziri wanatumika kwenye Bunge Tukufu kuwadanganya watanzania bila kuchukua hatua?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hii hoja ya mahabusu Kituo cha Kawe, tulishawahi kutoa maelekezo, uchunguzi ufanyike ili hatua ziweze kuchukuliwa, lakini kama Mheshimiwa Mbunge atataka kulithibitishia Bunge hili tukufu mpaka kama hatua hazijachukuliwa, basi nimuahidi kwamba nitakapotoka hapa nitafuatilia nijue ni kwa nini hatua kama hazijachukuliwa ama pengine wanastahili kuendelea kukaa ndani kwa mujibu wa sheria.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. Mwaka 2016 mwezi wa kumi, Mkoa wa Mara ndiyo walizindua REA Awamu ya Tatu na densification. Mpaka naongea sasa hivi, Jimbo la Tarime Mjini maeneo mengi, maeneo ya Kanyamanyori, Kata ya Nyandoto, Kitale na Nkende mradi huu haujaanza na ni kwa asilimia 90 hawa watu hawana umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua sasa ni lini Serikali itaenda kuelekeza maana imepita takribani miaka miwili ili miradi iweze kufanyika kwa ufanisi na wananchi waweze kupata umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko kuhusu masuala ya umeme katika Mkoa wa Mara hususan katika Jimbo lake, kwanza, kwa kuwa nimeona ndani ya Bunge bado changamoto za wakandarasi kuanza kuendelea na kazi, inaonekana Wabunge wengi hawaridhiki kwamba speed inaonekana ni ndogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge, mara baada ya kutupitishia bajeti yetu, sisi tunaendelea na ziara. Ndiyo maana leo Mheshimiwa Waziri hayupo, ameshafanya ziara pia katika Mkoa wa Mara. Kutokana na tatizo hili, naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba nitafanya ziara Mkoa wa Mara tena ili kuona kwa nini wakandarasi mpaka sasa hivi wanasuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba wakandarasi hili ni onyo la mwisho kwa kweli kama speed itaendelea Serikali ya Awamu ya Tano itasita kuvunja mikataba nao kKwa sababu miezi iliyobaki ni michache na tumeshawapa hela kwa nini inashindikana. Nashukuru ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Migogoro ya ardhi kati ya Jeshi na wananchi, kama alivyosema ipo nchi nzima, lakini nimekuwa nikizungumzia utatuzi wa mgogoro kati ya Jeshi la Wananchi na Mtaa wa Bugosi na Kenyambi kule Tarime ambao umedumu kwa muda mrefu sana na Mheshimiwa Waziri anaelewa; ni lini sasa Serikali itaona kwamba imeshindwa kupata fedha za fidia kuwalipa hawa wananchi, ukizingatia Jeshi la Wananchi limetoka kwenye Kambi yao, limekuja kwenye makazi ya wananchi?

Mheshimiwa Spika, kama hakuna fedha, tunaomba warudishe hii ardhi kwa wananchi ili waendelee na shughuli zao za maendeleo. Ni lini Serikali itawarudishia ardhi wananchi hawa wa Tarime?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna tatizo la mgogoro wa ardhi katika eneo hili la Tarime la muda mrefu, ninayo taarifa hii, tumeshazungumza mara kadhaa na Mheshimiwa Mbunge. Wataalam wameshauri na tathmini ya fidia imefanyika, kinachosubiriwa ni fedha ili ziweze kulipwa.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, katika mwaka huu wa fedha, bajeti yetu ilikuwa ni shilingi bilioni 20 katika kulipa fidia na upimaji wa ardhi katika maeneo mbalimbali. Bahati mbaya sana tumepokea kama shilingi bilioni tatu ambazo tumeshazilipa kule Kilwa, lakini mwaka wa fedha haujaisha, tuna matumaini kwamba fedha zitapatikana na zikipatikana tutaendelea kulipa katika maeneo haya ambayo uhakiki umeshafanyika.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Esther avute subira, ajue kwamba Jeshi nalo lina umuhimu wa kuwepo maeneo haya. Katika ulinzi wa nchi lazima tuone umuhimu wa taasisi hii ya Jeshi kuwepo. Siyo vizuri au siyo rahisi tu kusema kwamba kila ambapo tunashindwa kulipa fidia kwa wakati, basi Jeshi liondoke wananchi warudishiwe ardhi; ulinzi utafanywa na nani? Kwa hiyo, naomba subira iendelee na bila shaka tutalimaliza tatizo hili kwa haraka iwezekanavyo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa majibu yanayotia matumaini kama yatatekelezeka, kwa sababu mradi wa Ziwa Victoria kuanzia wakati wa Mheshimiwa Eng. Kamwelwe alisema mnafanya upembuzi yakinifu na mradi ungeenda kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mji wa Tarime ndiyo Makao Makuu ya Wilaya Tarime na umekuwa na matatizo ya maji kwa muda mrefu na kusababisha wananchi wasifanye shughuli zao za maendeleo; na kwa kuwa vyanzo vikuu katika Mji wa Tarime ni Bwawa la Nyanduruma na lile la Tagota ambalo halitoi majisafi na salama na Wizara tuliowaomba hata angalau wajenge treatment plant wakasema wanategema mradi mkubwa wa Ziwa Victoria:

Ni lini sasa mtahakikisha kwamba ule mradi ambao tumeuanzisha Gamasara ambao tumesha-rise certificate, Mkandarasi amesimama kuanzia Novemba tumeleta Wizarani mpaka leo hajalipwa, ni lini yule Mkandarasi atalipwa ili angalau ajenge lile tenki la lita 100,000 kuweza kusaidia wananchi wa Gamasara na Kata ya Nyandoto na Kata za pembezoni kwa kipindi hiki tukisubiria huu mradi wa Ziwa Victoria ambao mmesema unakwenda kuanza mwaka 2019/2020?

La pili, hawa DDCA wameshakamilisha na walileta certificate na hata Mheshimiwa Eng. Kamwelwe mimi mwenyewe nilimpa document, lakini mpaka leo inavyosemekana, hawajalipwa fedha na ndiyo maana hata hawajaanza kufanya huo utafiti wa maji ya chini ya ardhi kama mlivyo-report hapa. Napenda sasa nihakikishiwe leo kwamba hawa DDCA watalipwa fedha ili wananchi wa Tarime hasa zile Kata za pembezoni waweze kuchimba visima na wapate majisafi na salama. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimtoe hofu dada yangu Mheshimiwa Esther Matiko, Serikali ya Awamu ya Tano ikiahidi inatekeleza na ikichelewa kutekeleza, basi kunakuwa na sababu maalum ya kueleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ninalotaka kusema, pamoja na mradi mkubwa huo wa Ziwa Victoria katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji Tarime, lakini tuna mradi pale Gamasara wa asilimia 25, lakini tunatambua kabisa utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri, tulikuwa na madeni ya Wakandarasi zaidi ya shilingi bilioni 88, lakini tunamshukuru Mheshimiwa Rais amewaagiza watu Wizara ya Fedha kutupa zaidi ya shilingi bilioni 44 kwa ajili ya kuwalipa Wakandarasi na tumeshazipata na tumeshazigawa. Tuna shilingi bilioni 44 nyingine tutakazopewa mwezi huu wa Nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie, katika maeneo yote ambayo Wakandarasi wanadai, tutawalipa ili miradi iendelee kutekelezeka na ahadi ya kumtua mwana mama ndoo kichwani iweze kitimilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la DDCA, sisi pale tumeona haja ya uchimbaji wa visima. Sasa katika mgao huo wa shilingi bilioni 44, watu ambao wamelipwa ni watu wa DDCA. Tunawaagiza waende Tarime haraka katika kuhakikisha hii kazi inafanyika ili ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mwana mama ndoo kichwani inatimilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba endeleeni kutuunga mkono bajeti yetu katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama ilivyo ahadi kwa Jimbo la Bukene, Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni zake na hata Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne aliahidi kujenga barabara ya Tarime Mugumu ambayo ni kilometa 89 kwa kiwango cha lami; na kwa kuwa hii barabara ikijengwa itakuza uchumi siyo tu wa Tarime au Mara, bali wa Taifa, maana yake watalii watakao toka Kenya wataweza kupita kwenye njia ile:-

Ni lini sasa hii ahadi ya Mheshimiwa Rais itatimilika kwa kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Tarime Mugumu almaarufu kama Nyabwaga Road?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali iliahidi kujenga kipande cha kilometa 44 kutoka Tarime mpaka Mugumu kwa kiwango cha lami. Naamini hata Mheshimiwa Mbunge anajua kwamba upembuzi yakinifu ulishafanyika, usanifu wa awali ulishafanyika na usanifu wa kina ulishafanyika. Sasa hivi tunatafuta pesa kwa ajili ya kumpa Mkandarasi wa kujenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekitik, kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge awe na subira kidogo, tutajenda hiyo barabara kwa sababu ya umuhimu wa utalii wa nchi yetu kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Halmashauri ya Mji wa Tarime, kata zote zilikuwa haina kituo cha afya bali walikuwa wanategemea Hospitali ya Mji. Tunashukuru tumepata Kituo cha Nkende ambacho kinaendelea kujengwa; lakini kuna kata nne za pembezoni ambazo zina zahanati tu, kwa maana ya Kata ya Kitale, Kata ya Kanyamanyori na Nanyandoto. Wananchi wa katia ya Kanyamanyori wameamua kuchangishana ili kuendeleza kile kituo cha afya kwa maana kujenga maternity ward na maabara:-

Ni lini sasa Serikali itawatia moyo wananchi wale kwa kutoa fedha kuweza kujenga kituo afya cha ili kupunguza vifo vya mama na watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kutembelea Jimbo la Mheshimiwa Mbunge na nikatembelea Hospitali ya Wilaya ambayo mwanzo ilikuwa inahudumia maeneo mengi sana kiasi kwamba kukawa kuna congestion kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge mwenyewe anakiri na anashukuru kwamba kimeanza kujengwa kituo cha afya na imebaki hizo kata ambazo yeye amezitaja. Naomba aendelee kuiamini Serikali kwamba kama ambavyo tumeanza kujenga katika hiyo kata kwa kadri bajeti itakavyoruhusu, tumeahidi tutatekeza na katika kata nyingine kwa jinsi bajeti itakavyokuwa inaruhusu.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hospitali ya Wilaya ya Mji wa Tarime ambayo kiukweli inatoa huduma kama Hospitali ya Wilaya au ya Mkoa naweza nikasema na Kanda Maalum Tarime Rorya, Mheshimiwa Naibu Waziri alitembelea na akaona ni jinsi gani inaelemewa kwa utoaji wa huduma. Hivi ninavyoongea chumba cha kuhifadhia maiti kwa maana ya mortuary kwanza ni kifinyu lakini pia mashine yake kwa maana ya compressor haifanyi kazi na wale ndugu zetu ambao tunawahifadhi pale wakikaa muda mdogo wanaharibika. Nataka kujua commitment ya Serikali ya kuhakikisha kwamba inasaidia ukarabati au upanuzi wa mortuary ikiwemo kusaidia hiyo mashine ya compressor kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Tarime haina kipato cha kutosha. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge nilipata fursa ya kutembelea hospitali ile ambayo ina congestion kubwa na bahati nzuri nilipata fursa nikiambata na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Maelekezo ambayo yalikuwa yametolewa, kwanza ni kuhakikisha kwamba dawa za kutosha zinatolewa ili kukidhi haja kwa sababu wananchi ni wengi wanaopata huduma pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili ambalo amelisema kuhusiana na chumba hicho cha kuhifadhia maiti ambacho mashine imeharibika kiasi kwamba sasa mwili unaharibika ndani ya muda mfupi, naomba seriously tukitoka hapa tuwasiliane na Mheshimiwa Mbunge ili tuone hatua za haraka za kuchukua kuhakikisha kwamba mochwari ile inafanya kazi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuwa Serikali imekiri kwamba imetenga bilioni 12 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa hospitali za rufaa za mikoa na nafikiri na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara kwangu itakuwepo. Na kwa kuwa Serikali imekiri kwamba kuna ufinyu wa majengo katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora kupelekea hata vitanda kukosa sehemu ya kuweka na hivyo kupelekea msongamano wa wagonjwa na kudumaza utoaji wa huduma ya afya kwa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua sasa kati ya hizi bilioni 12 ni kiasi gani cha fedha kimetengwa specifically kwa ajili ya Hospitali hii ya Mkoa wa Tabora ili sasa kuondoa ufinyu wa majengo na kuweza kuondoa msongamano na vitanda viweze kupata mahala pa kuweka na wananchi wa Tabora waweze kupata huduma stahiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ni dhahiri kabisa inatambulika kwamba tuna uhaba wa wauguzi kwa maana ya madaktari, manesi na madawa katika hospitali zetu nyingi nchini. Na tunatambua kwamba uhaba huu umepelekewa na sababu mbalimbali ikiwepo zoezi la vyeti feki ambalo Serikali ya Awamu ya Tano iliendesha, vifo na kustaafu. Hospitali yangu ya Mji wa Tarime ina ukosefu wa daktari ni wengi lakini specifically daktari wa meno ambaye amefariki kuanzia mwaka jana na nimekuwa nikiongea hapa. Ningetaka kujua sasa ni lini Serikali itaweza kutuletea daktari wa meno ili wananchi wa Tarime waendelee kupata huduma hii ya meno?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza specifically kiasi gani ambacho tumekitenga katika Hospitali ya Rufaa ya Mko wa Tabora hususan katika kuboresha miundombinu ile. Hiyo data sinazo hapa kwa hiyo nitamwomba tu Mheshimiwa Mbunge tukishamaliza kikao hichi tuongee na watendaji wetu ili waweze kutupatia hizo taarifa na niweze kumpatia taarifa ambayo kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili ameulizia kuhusiana na daktari wa meno ni kweli Serikali imekuwa inaendelea na jitihada za kuziba mapengo wa vyeti feki na zile ajira nyingine. Na katika awamu ya kwanza tuliajiri takribani watumishi 3152 kuziba pengo la watumishi feki na Serikali baadaye ikaongeza watumishi takribani 8000 na sasa hivi tuko katika hatua za mwisho kuangalia hawa ambao walistaafu, wamefariki ili nao nafasi zao ziweze kuzibwa na tuko katika hatua za mwisho kabisa kuweza kuziba haya mapengo ya wale ambao wamefariki na wamestaafu ili sasa nafasi zao ziweze kujazwa. Na nikuhakikishie kwamba Tarime huyo daktari ambaye wamemwitaji wa meno naye atapatikana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa sasa tunajua kwamba tuna mradi wa REA ambao ndiyo umejielekeza kupeleka umeme vijijini. Katika Kijiji cha Sazira katika Jimbo la Bunda Mjini ambalo lina Vitongoji vitatu cha Nyamungu, Wisegere na Kinamo havijawahi kupitiwa na mradi huu wa REA phase I, phase II na hata phase III. Sasa ningependa kujua hawa wananchi wa Kijiji cha Sazira ni lini watapatiwa umeme ili na wenyewe waweze kupata umeme katika shughuli zao za kimaendeleo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika Mji wa Tarime pia tumepitiwa na umeme wa REA ambao unapita kwenye aidha Kijiji sehemu ndogo tu au kata. Ningependa kujua maeneo ambayo yana Taasisi kama sekondari, zahanati au vituo vya afya na shule ya msingi kama vile Kitale tuna Kijiji cha Nkongole ambacho kina hizo Taasisi zote, Kenyamanyori Senta tuna Kibaga ambayo ina mgodi pale haijapitiwa na umeme wa REA. Ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba inapeleka huu umeme wa REA kwenye yale maeneo ambayo hayajaguswa kabisa na Mheshimiwa Naibu Waziri aliniahidi kwamba ungeweza kwenda Tarime kujihakikishia hayo maeneo ambayo kila siku nayauliza hapa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ameulizia Kijiji cha Sazira ambacho kipo Bunda Mjini ambacho kina vitongoji vitatu na hakina umeme. Kama ambavyo tumepata kujibu maswali hapa ya msingi kwamba mpango wa Serikali ni kupeleka umeme vijiji vyote. Kwa sasa tuna mradi huu unaoendelea wa REA awamu ya tatu ambao unahusisha vijiji 3,559 lakini ukichanganya na miradi mingine yote ya Ujazilizi, BTIP tunatarajia kufikisha umeme ifikapo Julai, 2020 kwa vijiji 9,299.

Kwa hiyo kijiji ambacho amekitaja kwenye Wilaya ya Bunda Mjini hapo vipo katika mpango wa REA awamu ya tatu, mzunguko wa pili ambao utaanza Julai, 2019 na kukamilika 2021. Kwa hiyo niwatoe hofu tu wananchi wote nchi nzima, mpango wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kupeleka umeme katika vijiji vyote nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameulizia suala la Jimbo lake la Tarime; ni kweli niliahidi kutembelea Jimbo hilo kama utaratibu wetu ndani ya Wizara, lakini nitazingatia angalizo lako kwamba kwa ruhusa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini nimtoe hofu tu Mheshimiwa Esther kwamba katika maeneo ambayo ameyataja na hasa Taasisi za Umma, Wizara imetoa maelekezo mahususi na naendelea kurejea hayo maelekezo kwamba Taasisi za umma ni moja ya kipaumbele katika kuzipelekea umeme iwe shule ya msingi, sekondari, kituo cha afya au miradi ya maji.

Kwa hiyo naomba niwaelekeze Wakandarasi kuzingatia maelekezo hayo na Mameneja wote wa TANESCO na wasimamizi wa miradi hii ya REA kwamba umeme ufikishwe kwenye Taasisi za Umma ili kuboresha utoaji wa huduma ambazo zinatokana na hizo Taasisi za umma.

Mheshimiwa Spika, katika haya maeneo aliyoyasema Mheshimiwa kwanza mojawapo lipo katika REA awamu ya tatu, mradi unaoendelea na Mkandrasi Derm yupo, anaendelea vizuri na ni moja wa Wakandarasi ambao kwa kweli wanafanya kazi vizuri na nimhakikishie tu mpaka Juni, 2019 hii miradi itakuwa imekamilika. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ni dhahiri kwamba Serikali imekuwa haitoi kipaumbele kwenye huduma muhimu za binadamu badala yake wamekuwa wakiwekeza zaidi kwenye vitu.

Mheshimiwa Spika, magereza ni moja ya sehemu ambazo inatakiwa wapewe vipaumbele na wapewe huduma stahiki kama inavyoelekeza. Wazabuni wengi wanadai na wameacha kutoa huduma za vyakula na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha zaidi nilitaka nijue, Serikali ni lini itatoa nguo kwa wafungwa ambao mnasema kabisa wakishafungwa wavae yale mavazi. Niliona hiyo nikiwa Segerea, lakini juzi nilivyotembelea Gereza la Tarime pamoja na matatizo mengi ambayo yametokana na kutokulipa madeni ya wazabuni na kuweza kutoa vifaa hivi unakuta mpaka Askari Magereza anachukua nguo zake anavisha mfungwa kama anavyotoka nje.

Ni lini sasa Serikali itaondoa hii fedheha ihakikishe kwamba wafungwa ambao wanastahili kuvaa nguo waweze kupewa zile nguo ambazo wataweza kujihifadhi? Na wajue kabisa kwamba waliopo Serikalini leo magereza ni yao kesho. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimsahihishe siyo sahihi kwamba Serikali haitoi kipaumbele kwenye huduma mbalimbali ikiwemo za wafungwa. Nimhakikishie kwamba wafungwa hawa tumekuwa tukiwapatia uniform na siyo wote kama ambavyo umetaka ieleweke kwamba hawana uniform, lakini changamoto hii itaendelea kupungua hatua kwa hatua. Hata hivyo, sehemu kubwa ya wafungwa tayari wameshaanza kupatiwa nguo kwenye magereza.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wananchi wa Mji wa Tarime wameendelea kupata adha kubwa ya maji safi na salama na hasa upatikanaji wake. Kupitia Bunge hili nimeshauliza maswali mengi sana na kuchangia na Serikali ikaahidi kwamba, itatoa suluhisho la muda mfupi la kuchimba visima 23 kandokando ya Mji wa Tarime kuweza kuboresha Mradi wa Gamasara na Bwawa la Nyanduruma, lakini zaidi kwenye bajeti iliyopita waliahidi Mradi wa Ziwa Victoria ambao unatokana na mkopo kutoka India kwamba, unaenda kuanza ambao ni suluhisho la muda mrefu.

Sasa napenda kupata majibu kutoka kwa Naibu Waziri, ni lini sasa hii miradi yote inaenda kutengemaa ili wananchi wa Mji wa Tarime waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, dada yangu Esther Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tuna Mradi pale wa Gamasara ulikuwa ukifanya kazi kwa kusuasua, nilifika na tumechukua hatua kubwa ya kushughulikiana na yule mkandarasi. Wiki hii tunafunga pampu ili kuhakikisha wananchi wale wanapata huduma hii ya maji, lakini tunatambua kabisa Mkoa wa Mara ni maeneo yenye changamoto.

Mheshimiwa Spika, tumepata fedha takribani kwa mikoa 17 mmojawapo ukiwa Mkoa wa Mara na tumekwishatuma fedha zaidi ya Sh.8,345,000,000. Katika jimbo lake mpaka sasa tumekwishatuma pesa zaidi ya Sh.1,345,000,000, hizo fedha ni kwa ajili ya utekelezaji. Kwa hiyo, hizo fedha ziende zikatumike katika kuhakikisha zinachimba visima katika maeneo yenye changamoto ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia katika kuhakikisha tunatatua kabisa tatizo la maji Rorya pamoja na Tarime ni moja ya maeneo ambayo tumeyaweka katika miji 28 kupitia fedha za India. Tunasubiri kibali kutoka Exim Bank ili tuweze kutangaza tenda kwa ajili ya kuwapata wakandarasi na Mradi ule mkubwa wa kuyatoa maji Ziwa Victoria ili wananchi wa Tarime waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwanza napenda kumshukuru Naibu Waziri maana tarehe 07 Agosti, alikuja Wilaya ya Tarime na kuna maagizo aliyatoa kwenye Mradi wa Gamasara na wa Nyanduluma, lakini nataka kujua ni lini sasa vile visima 23 ambavyo Bunge lililopita niliuliza hapa na ukaelekeza kwamba, ni DCA wanaenda kuanza kuvichimba mara moja, lakini mpaka sasa hivi hamna chochote ambacho kinaendelea kwenye Jimbo la Tarime Mjini, ili kuweza kutoa suluhisho la la muda mfupi wakati tukisubiri ule mradi wa Ziwa Viktoria? Ahsante?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, nikiri nimefika Tarime na moja ya changamoto kubwa kiukweli changamoto kubwa ipo pale Tarime. Na moja ya changamoto ambayo tumeona jambo la kulifanya haraka kwanza tume-terminate mkataba wa yule mkandarasi wa Mradi wa Gamasara, mradi ule tutaufanya kwa sisi wenyewe kuwapatia fedha wataalam wetu waweze kuutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna suala la uchimbaji wa visima. Tumekwishawaagiza watu wa DDCA na sisi tumejipanga kuwapatia fedha ili uchimbaji wa visima 23 uweze kuchimbwa pale wakati tunasubiri mradi mkubwa wa fedha zile za India. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wa Tarime kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Adha iliyopo Urambo ya Hospitali ya Wilaya kuhudumia population nje ya eneo linalohitajika ni sawa na ile ya Hospitali ya Mji wa Tarime ambayo kwa kweli na nimeshaongea mara nyingi sana hapa Bungeni, inahudumia watu nje ya population ya Mji wa Tarime, wanatoka Shirati, Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na Serengeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Kata ya Kinyemanyoli waliamua kujenga kituo cha afya ili kupunguza ile population ambayo inaenda kupata huduma ya Halmashauri ya Mji wa Tarime na nilishauliza hapa akaahidi kwamba angeweza kupeleka fedha. Nataka kujua sasa ni lini Serikali itapeleka fedha ku-support nguvu za wananchi ili tuweze kuwa na kituo cha afya Kinyemanyoli kupunguza adha wanayopata wajawazito na watoto?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri kwa maswali yaliyoulizwa hapo awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu Mkoa wa Mara umekuwa na changamoto mbalimbali za sekta ya afya lakini tumefanya investment kubwa katika mkoa huo na tukifahamu kwamba eneo la Tarime Mji napo kuna changamoto hizo. Ni jukumu la Serikali kuangalia nini kifanyike katika maeneo hayo kama tulivyofanya kazi katika Mkoa mzima wa Mara. Kwa mfano, kwa sasa hivi tunajenga Hospitali za Wilaya takriban tatu na kuimarisha vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Esther Matiko kwamba tunaifahamu changamoto zilizopo kule na tunazishughulikia. Kikubwa zaidi naomba nimuagize Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mara kwenda kufanya tathmini na kutuletea taarifa ili katika mchakato wetu wa bajeti unaokuja mwezi wa tano tuangalie jinsi gani tutaweza ku-address matatizo ya maeneo hayo kwa sababu lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba wananchi wa Tarime Mji wanapata huduma vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo tu kwamba wanadhurika vijana mahabusu kwa kuona tabia za wale wafungwa wabakaji, wezi na madawa ya kulevya lakini tumeshuhudia akina mama wanakuja wajawazito wanajifungulia gerezani, kuna akina mama wanakamatwa wakiwa na watoto wanakuwa nao gerezani wanachangamana na hao watu ambao wanatabia za tofauti tofauti na tunajua kabisa kwamba mtoto mchanga kuanzia zero age mpaka five years anakuwa ndiyo muda ambao anajifunza na kuweza kuweka vitu akilini, mtoto yule anakua kwenye makuzi ya gerezani anafuata zile tabia ambazo hazina maadili kabisa.

Je, Serikali ni kwa nini sasa isitafuta mbadala kama inashindwa kuwapa dhamana hawa mahabusu wenye watoto ni kwanini isitenge sehemu kabisa ya wamama wajawazito na wamama wanaonyonyesha waweze kukaa na wale watoto mpaka watakapofikia umri wa kuweza kuwatoa gerezani, kuliko kuchangamana wanaona wale akina mama saa nyingine wako uchi, wako hivi ni tabia mbaya na haiwatendei haki hawa watoto. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto hawa wanaruhusiwa kuchukuliwa na familia zao, kwa hiyo, watu wengi ambao wanafungwa, wakinamama ambao wana watoto wanapofikia umri baada ya kuacha kunyonyesha, mara nyingi huchukuliwa na jamaa zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa wale ambao watakuwa wanaendelea kubakia magerezani aidha kwa sababu ya kukosa jamaa wa kuwaangalia nje, kuna utaratibu mzuri ambao unaandaliwa na mimi binafsi nimetembelea magereza mengi sana na ninapotembelea kwenye magereza hayo hutembelea katika maeneo ya wanawake na katika mambo ambayo tunaangalia moja ni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahakikisha kwamba watoto wale wanapata elimu, wanaandaliwa mazingira mazuri na wanasoma katika shule za nje ya gereza. Kwa hiyo, kimsingi jambo hili tunaliangalia kwa uzito wa aina yake ili kuhakikisha kwamba watoto wale hawapati madhara ya kisaikolojia wakati wanapokuwa gerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niendelee kutoa wito kwa wakinamama kujiepusha na kufanya vitendo vya kiharifu ili kuepusha kuwaingiza katika matatizo watoto hawa hasa wanapokuwa katika umri mdogo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, Mji wa Tarime tuna Migodi midogo ya Buguti na Kibaga, tumekuwa tukishuhudia migogoro kwa wachimbaji wadogo kwenye mgodi wa Kibaga na Mgodi ule wa Kibaga leseni yake iko na Barrick kwa muda mrefu na nimeshawahi kuuliza hapa, Serikali ikasema kwamba ina- revoke leseni ya Barrick. Na kwa sababu leo Naibu Waziri imekiri kwamba zile leseni zote ambazo hazifanyiwi kazi mtaenda kuzifuta na kuwapa wachimbaji wadogo. Ningetaka kujua specifically, kwa wachimbaji wadogowadogo wale wa Kibaga, ni lini sasa ile leseni itaondolewa kwa Barrick ili waweze kupewa wachimbaji wadogowadogo wa Kibaga waweze kufanya kazi zao kwa ufasaha zaidi na bila kubughudhiwa?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tumekwishakutoa tamko, kwa leseni zote ambazo hazifanyiwi kazi, na hasa ambazo ziko kwenye utafiti na hazifanyiwi kazi, zirejeshwe, zirudishwe na sisi tuweze kutafuta namna ya kuwagawia wachimbaji wadogo na tunawagawia katika vikundi. Mheshimiwa Mbunge ameniuliza swali hilo lakini hakunipa specific namba ipi, naomba tu nilichukue suala hili, tuone ni leseni ipi, aidha ni ya uchimbaji, au ni leseni ya utafiti. Kama leseni ni ya utafiti na haifanyiwi kazi, sisi tutazirudisha, lakini nimhakikishie tu kwamba kuna leseni nne ambazo zilisharudishwa na watu wa Barrick maeneo hayo na wameshaturudishia sisi na walishaandika barua, tutaangalia namna ya kuangalia kuwagawia wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu, ameonesha m ikakati iliyopo kwa Butiama, Kiabakari, Mugango na Vijiji 13 vya Musoma Vijijini lakini katika swali la msingi la Mheshimiwa Sokombi aliweza kuonesha adha ya maji Mkoa wa Mara na akataja na Serengeti. Ningependa kujua mkakati uliopo kwa Wilaya ya Serengeti hasa maeneo ya vijijini ambayo kwakweli wananchi wa pale hawana maji kabisa. Ni mkakati gani Serikali mko nao ikiwemo wa kupeleka visima maeneo ya Serengeti Vijijini, sio pale Serengeti Mji. Mkakati gani upo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili mwezi wa tatu wakati Mheshimiwa Naibu Waziri ukijibu swali langu kuhusiana na adha ya maji Tarime kwa muda mfupi wakati tukisubiria mradi unaotoka ziwa Victoria, niliweza kuulizia vile visima 23 ambavyo Serikali ilisema itakuja kuchimba na DDCA alikuwa ameshafanya usanifu wa awali. Ulinihakikishia kwamba sasa tatizo lilikuwa ni hela na ukaagiza DDCA waende. Lakini ninavyoongea sasahivi ni takriban mwezi mmoja na nusu unaenda bado DDCA hawajafika katika Tarime Mji kuhakikisha kwamba wanatuchimbia vile visima 23 wananchi wa maeneo ya pembezoni waweze kupata maji tukisubiria Mradi wa Ziwa Victoria.

Ni lini sasa wataenda? Maana mpaka sasa hivi DDCA hawajaenda. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, dada yangu lakini kikubwa ninachotaka kukisema sisi kama Wizara ya Maji tunatambua changamoto, si Serengeti tu kwa maana ya Mkoa wa Mara na ndiyo maana katika Miji 28 ambayo tumeiorodhesha kwa ajili ya kutatua tatizo la maji tumeipa kipaumbele zaidi ya miji mitatu kwa maana ya Tarime, Mugumu ambayo ipo Serengeti lakini pia Rorya katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nikuhakikishie tumekwishasaini mkataba katika kuhakikisha utekelezaji huu unakwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia yale maeneo ambayo yapo kandokando na Ziwa Victoria hususan Vijijini tunafanyia usanifu ili kuhakikisha vijiji vile ambavyo vipo pembezoni na Ziwa Victoria ili viweze kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la uchimbaji visima katika Jimbo lako la Tarime tulikwishaagiza na tumepewa agizo hilo kuhakikisha kwamba linatekelezeka lakini kuna mabadiliko tu ya kiutendaji katika Wakala wetu wa Maji na wa Uchimbaji Visima DDCA lakini sasa hivi ameshapatikana Mkurugenzi, tunamuagiza kwa mara nyingine aende kuchimba visima vile ili wananchi wale waeze kupata maji. Kuhusu mradi wako wa Salasala pia tumekwishawalipa. Tunamtaka mkandarasi atekeleze m radi ule na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Mji wa Tarime kwa hadhi ya kuwa mji ulitakiwa kuwa na umeme kwa zaidi ya asilimia 90, lakini maeneo yenye umeme ni chini ya asilimia 40. Na kwa sababu, Waziri wakati anajibu baadhi ya maswali hapa amehakikisha kwamba, na akatoa instructions kwamba, vituo vya afya, zahanati, shule kama sekondari vihakikishwe vinapewa umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo langu Kata ya Nkende kuna kituo cha afya, kuna sekondari na kuna shule za msingi, lakini hazina umeme. Kata ya Kenyamanyori ina shule ya sejkondari, ina shule za msingi, ina kituo cha afya hakina umeme na Kata ya Kitale kuna Sekondari ya nkongole na Mogabili na vituo vya afya pale, zahanati hazina umeme, vilevile na Kata ya Nyandoto.

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua sasa ni lini, na nimekuwa nikiuliza haya maswali, ni lini huu umeme wa REA utaweza kufika kwenye hayo maeneo ambayo hayana umeme kabisa, ili sasa hizo zahanati, vituo vya afya, sekondari na shule za msingi ziweze kupata umeme, pamoja na Wananchi? Ahsante.
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza pamoja na kuwapongeza Wananchi wa Tarime kwa kupelekewa umeme katika vijiji vyote iko changamoto katika kata ambazo amezitaja, hasa Kata ya Nkende pamoja na Kenyamanyori na Kitale. Nimeshazungumza mpaka na Mkurugenzi alipie zahanati na shule zipelekewe umeme kwa sababu, vijiji na vitongoji vya maeneo hayo vina umeme. Kwa hiyo, nikupongeze Mheshimiwa kwa kufuatilia, lakini nikuombe uwasiliane na Mheshimiwa Mkurugenzi na Halmashauri ya Kijiji cha Nkende pamoja na Kijiji cha Kitale na Kenyamanyori waweze kulipia ili shule na zahanati zipelekewe umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, nyongeza ya hilo, nitapenda nitembelee mimi mwenyewe ili nikatoe maelekezo kwa wakurugenzi waweze kulipia. Mheshimiwa Esther hata akibaki nitakwenda mwenyewe ili kusudi maeneo hayo na zahanati ziweze kupatiwa umeme, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nisikitike kwa majibu ya Serikali ambayo yametolewa na Naibu na Waziri sasa hivi Serikali ya Awamu ya Tano tunasema tunaelekea kwenye Tanzania ya Viwanda na kwa kasi kubwa sana ununuzi wa ndege ambao tuahitaji pilot na Ma-engeneer, mnajenga SGR, stiegler’s gorge zote zitahitaji wataalam.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya majibu hayatoi uhalisia ni mwezi Mei mwaka huu tumepewa mwalimu mmoja wa sayansi sasa kama Mheshimiwa Naibu Waziri anazungumzia walimu toka Tanzania tupate uhuru kweli tunao walimu 59, na upungufu ni mkubwa. Maswali yangu sasa.

Ningependa kujua katika sekondari tisa ambazo zipo ndani mji wa Tarime ni sekondari mbili ambayo ni High School ya Tarime na sekondari ya Mogabili ndio maabara zimekamilika sekondari saba zote maabara hazikamilia majengo ni yale ambao wananchi wamejenga na kwa kufanya hivi inazorotesha ufaulu wa wanafunzi. Ningependa kujua Serikali ni lini mtaleta fedha ili tuweze kukamilisha maabara ya hizi sekondari saba ambazo hazijakamilika zikisubiri Serikali ikamilishe pamoja na vifaa?

Katika Halmashauri ya Mji wa Tarime tuna sekondari moja tu A-Level na kama unavyojua kwamba tuna sekondari tisa. Wanapomaliza form four wanafunzi wetu wengi na hasa wasichana wanashindwa kupata nafasi kuendelea na high school. Ni lini sasa Serikali itapandisha hadhi walau Mogabili Sekondari au Nyandoto kuwa A-level nayo ili kuchukua wanafunzi mchanganyiko kwa maana wavulana na wasichana ili watoto wetu wa kike waweze kwenda High School?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upole kabisa haya ndio majibu ya Serikali, yeye Mheshimiwa Esther kama ana majibu yake nadhani abaki nayo. Majibu ya Serikali majibu haya yanaandaliwa kutoka Halmashauri ya Tarime. Hakuna taarifa za uwongo ambazo zinatolewa hapa mbele ya Bunge letu Tukufu na ndio taarifa ya hali halisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili suala la kupeleka walimu na kupeleka vifaa vya maabara haliwezi kabisa kulinganishwa na miradi mingine ya maendeleo kwa sababu kila kitu kinajitegemea na vyote ni muhimu sana na vinafanyika sambamba. Tumeajiri walimu awamu hii ya juzi 4500 ndio imepata walimu wachache, awamu iliyopita walimu walipelekwa Tarime lakini bahati nzuri na mimi nimefika wanazungumza ukifika Tarime pale tunazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala shule kupandishwa hadhi Waheshimiwa Wabunge mnafahamu ni suala la mchakato ni lazima ninyi wenyewe kama Mbunge wa eneo husika kupitia halmashauri yako kupitia vikao vya halmashauri kamati ya fedha, bajeti ya ndani na wadau mbalimbali ikiwepo na mfuko wako wa jimbo mleta maoni TAMISEMI Wabunge walioleta maoni yakupandishwa shule zao kuwa high school yanafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ninaomba nitoe taarifa kuanzia mwezi mwaka huu tuna shule nyingi zinaanzishwa ambao tumepata maoni kutoka kwa Wabunge wenyewe kwa vyanzo vya ndani tumpelekee Serikali na walimu tunawapeleka katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante; ni dhahiri kwamba Watanzania wengi ambao unakuta wamemaliza kidato cha sita na wengine ambao wanasifa za kwenda vyuo vikuu wanatamani sana kupata mikopo ya elimu ya juu ili tuweze kuwa na wataalam wa fani mbalimbali. Mikopo hii inapotolewa tumeweka riba kubwa sana ya asilimia kumi na tano ambayo ipo katika sheria ya 2016 na penati ya asilimia sita. Hivyo, tunakuta wanufaika wengi ambao ni watoto wa familia maskini wanashindwa kulipa au kubeba huu mzigo. Je, ni lini sasa Serikali italeta mabadiliko ya sheria hii angalau tupeleke kwenye singledigit kwa maana ya asilimia nane au tano ili tuwe na lengo la kutoa wajuzi na siyo kugeuza kama chanzo cha mapato? Ahsante.(Makofi)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza swali lake la nyongeza ukiangalia kwa kiasi kikubwa haliendani na swali la msingi, lakini kwa sababu ya umuhimu wa masuala ya Bodi ya Mikopo, ningependa kwanza kuonesha kwamba mwombaji wa kwanza anasema wanafunzi wote wapate mikopo, lakini mwombaji wa pili anasema makusanyo wapunguze.

Mheshimiwa Spika, lengo la kuanzisha Mfuko huu wa mikopo ilikuwa ni kwamba watu wafanye marejesho, mikopo ijiendeshe yenyewe kama vile revolving fund yaani yale marejesho yakikusanywa yatosheleze kuwapatia wanafunzi wengine. Kwa hiyo, ukiangalia hata sasa makusanyo ya mikopo yanachangia asilimia 46 ya bajeti ya mikopo. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba umuhimu wa kurejesha mikopo upo na asilimia 15 ambayo mwanafunzi anakatwa, anabaki na asilimia 85 ya mkopo wake, tukumbuke kwamba mkopo wa Bodi ya Mikopo ndiyo uliotangulia kabla ya mikopo mingine na Kanuni za Utumishi makato ni kwamba mtumishi anatakiwa abaki na theluthi moja ya mshahara.

Mheshimiwa Spika, nawasihi wanaochukua mikopo, waone umuhimu wa kulipa na wale wenye fedha wasisubiri kukatwa hiyo asilimia kumi na tano, kumi na tano ili wanafunzi wengine waweze kunufaika kama wao walivyonufaika, wakaweza kupata ajira. Kwa hiyo naomba sana Waheshimiwa Wabunge watusaidie kutoa elimu kuonesha umuhimu wa kurejesha mikopo kwa sababu marejesho hayo ndiyo yanawasaidia wengine kupata mikopo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante; ni dhahiri kwamba Watanzania wengi ambao unakuta wamemaliza kidato cha sita na wengine ambao wanasifa za kwenda vyuo vikuu wanatamani sana kupata mikopo ya elimu ya juu ili tuweze kuwa na wataalam wa fani mbalimbali. Mikopo hii inapotolewa tumeweka riba kubwa sana ya asilimia kumi na tano ambayo ipo katika sheria ya 2016 na penati ya asilimia sita. Hivyo, tunakuta wanufaika wengi ambao ni watoto wa familia maskini wanashindwa kulipa au kubeba huu mzigo. Je, ni lini sasa Serikali italeta mabadiliko ya sheria hii angalau tupeleke kwenye singledigit kwa maana ya asilimia nane au tano ili tuwe na lengo la kutoa wajuzi na siyo kugeuza kama chanzo cha mapato? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza swali lake la nyongeza ukiangalia kwa kiasi kikubwa haliendani na swali la msingi, lakini kwa sababu ya umuhimu wa masuala ya Bodi ya Mikopo, ningependa kwanza kuonesha kwamba mwombaji wa kwanza anasema wanafunzi wote wapate mikopo, lakini mwombaji wa pili anasema makusanyo wapunguze.

Mheshimiwa Spika, lengo la kuanzisha Mfuko huu wa mikopo ilikuwa ni kwamba watu wafanye marejesho, mikopo ijiendeshe yenyewe kama vile revolving fund yaani yale marejesho yakikusanywa yatosheleze kuwapatia wanafunzi wengine. Kwa hiyo, ukiangalia hata sasa makusanyo ya mikopo yanachangia asilimia 46 ya bajeti ya mikopo. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba umuhimu wa kurejesha mikopo upo na asilimia 15 ambayo mwanafunzi anakatwa, anabaki na asilimia 85 ya mkopo wake, tukumbuke kwamba mkopo wa Bodi ya Mikopo ndiyo uliotangulia kabla ya mikopo mingine na Kanuni za Utumishi makato ni kwamba mtumishi anatakiwa abaki na theluthi moja ya mshahara.

Mheshimiwa Spika, nawasihi wanaochukua mikopo, waone umuhimu wa kulipa na wale wenye fedha wasisubiri kukatwa hiyo asilimia kumi na tano, kumi na tano ili wanafunzi wengine waweze kunufaika kama wao walivyonufaika, wakaweza kupata ajira. Kwa hiyo naomba sana Waheshimiwa Wabunge watusaidie kutoa elimu kuonesha umuhimu wa kurejesha mikopo kwa sababu marejesho hayo ndiyo yanawasaidia wengine kupata mikopo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali imekiri kabisa kwamba wananchi wa Tarime asilimia 20 ndiyo wanaopata maji. Tatizo la maji ni Tanzania nzima. Sasa napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa miradi ya muda mfupi; visima virefu, Mradi wa Bwawa la Nyanduma ambalo tumekuwa tukilitengea fedha lakini haziendi na miradi mingine kama ya Gamasala na kwingineko kwa Tarime Mji, napenda kujua, ni lini Serikali itaenda kuchimba vile visima 23 ambavyo wameahidi kuanzia mwaka 2016 viweze kuwa suluhisho la muda mfupi kwenye Kata ya Kitale, Nyandoto, Kenyamanyoli na Mkende wakati tunasubiria Mradi wa Ziwa Victoria? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, jana wakati wameweka Mpango hapa, Serikali imekiri kabisa kwamba imepeleka maji vijijini kwa asilimia 70.1, wamechimba visima miradi 1,423 ambapo kuna vituo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Esther, naomba uulize swali tafadhali.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Miradi hiyo ina vituo 131,000. Kwa Rorya tuna mradi mkubwa kule Kirogo ambao umetumia zaidi ya shilingi bilioni 1.3, ulitakiwa kuwa na vituo 23…

NAIBU SPIKA: Swali Mheshimiwa.

MHE. ESTHER N. MATIKO: … lakini kuna vituo vitatu tu ambavyo vinatoa maji. Ni lini sasa Serikali itahakikisha maji yanatoka kule Kirogo kwa vituo vyote 23 na siyo vituo vitatu tu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuhakikisha wananchi wote wanapata maji safi, salama na ya kutosheleza kwa maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania. Hivi karibuni Mheshimiwa Waziri alikuwa ziarani hapo Tarime na aliweza kuwasiliana na kuambatana na Mbunge wa Tarime Mjini ambaye ni Mheshimiwa Kembaki na Mbunge wa Tarime Vijijini, Mheshimiwa Naibu Waziri Waitara na Mheshimiwa Waziri ametoa ahadi hivyo visima vyote vitachimbwa ndani ya kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa kuanza, katika mwaka wa fedha ujao, visima vitachimbwa na maji safi na salama yatapatikana bombani kwa wananchi wote wa Tarime. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kama nilivyojibu kwenye jibu langu la awali ambalo ni jibu langu la msingi. Eneo la Rorya visima hivi vitatu kwa sasa hivi vinapata maji kati ya 27. Vijiji hivi vinakwenda kupatiwa huduma kupitia Mwaka wa Fedha 2021/2022 lakini vile vile tayari Wahandisi wetu wa eneo lile wanaendelea na hii kazi na visima vile ambavyo vilisalia vinakwenda kuchimbwa na kuhakikisha kuona kwamba vinakwenda kutoa maji ya kutosheleza kwa wananchi wote wa Rorya.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wananchi wa Mtaa wa Kenyambi na Bugosi katika Mji wa Tarime wana mgogoro wa muda mrefu na Jeshi la Wananchi na Serikali imeshafikia hatua nzuri tu ya kufanya tathmini na ikarudia tena kufanya tathmini bado imebakiza malipo. Napenda kujua ni lini wananchi wale wataenda kulipwa fidia yao ili waweze kuondoka maeneo yale na kuwaachia Jeshi la Wananchi wa Tanzania? (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru kwa kutambua kwamba tunaendelea kuwajali wananchi wetu wa Tanzania na niseme tu kwamba migogoro hii ilikuwepo kadhaa lakini niseme kwamba kati ya migogoro hiyo, zaidi ya asilimia 50 ya migogoro tumeshaitatua. Yako maeneo ambayo tumeyatambua kwa ajili ya fidia na wananchi wameshalipwa, yapo maeneo mengi ambayo tayari tumeshalipa. Hii inaonesha tunao mwendelezo mzuri wa kuendelea kulipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wananchi hawa wa Tarime wavute subira kwa sababu tunatafuta fedha. Tukipata fedha kwa maeneo yote ambayo tumeyatambua yanahitaji fidia kwa wananchi wetu tutakwenda kuwafanyia malipo. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge kuvuta Subira na wakati mwingine tunaweza tukaonana ili nimueleze kwa kinagaubaga namna tunavyokwenda kutatua matatizo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Kicheko)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Matatizo yaliyopo katika Wilaya ya Butiama Mkoa wa Mara yanaonyesha uhalisia wa Wilaya zote ndani ya Mkoa wa Mara kwenye kadhia ya umeme na kwa sababu umeme unaweza kuimarisha usalama na kuweza kukuza uchumi kwa maana kupitia uanzishwaji wa viwanda na vitu vingine. Ningependa kujua ni lini sasa Serikali itahakikisha umeme unapatikana katika wilaya zote ndani ya Mkoa wa Mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wilaya zote Tanzania Bara zina umeme, maeneo machache katika wilaya hizo ndiyo hayajafikiwa na umeme, kwa hiyo nimhakikishie kwamba maeneo hayo machache ambayo bado hayajafikiwa na umeme kwa maana ya vijiji yatakuwa yamepatiwa umeme katika miezi 18 ijayo. Kama ni umeme wa uhakika kama nilivyotangulia kujibu maswali yaliyotangulia ya msingi, Serikali inaendelea kuwa na jitihada za kuhakikisha inatenga bajeti kuhakikisha inawawezesha TANESCO kuendelea kurekebisha miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, pia Serikali inatekeleza miradi mikubwa sana ya ufuaji wa umeme Tanzania bara ikiwemo ya Mwalimu Nyerere itakayozalisha megawatt 2,115, Rusumo megawatt 80, Kagati megawatt 14, Ruhudji megawatt 358 na Rumakali megawatt 222. Miradi yote hiyo ikikamilika tutaweka umeme mwingi sana kwenye grid yetu ya Taifa na kuweza kumpatia kila mmoja umeme wa kutosha. Kwa hiyo tunawahakikishieni Wabunge wote kwamba umeme upo na utaendelea kuongezwa, tutarekebisha miundombinu yetu ili kila moja aweze kufikiwa na umeme ili Tanzania ya viwanda iweze kuwa ya kweli.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali imeweza kutoa fedha nyingi sana za walipa kodi masikini kwenda kwenye miradi ya maji, lakini uhalisia ni kwamba miradi mingi sana haitoi maji kwa ukamilifu au mingine haitoi maji kabisa. Ningependa kujua, ni lini Serikali itafanya ukaguzi kwenye miradi yote nchi nzima ambayo haitoi maji ili sasa iweze kutubainishia bayana ni miradi ipi kwa fedha kiasi gani zimewekezwa na haitoi maji kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli fedha nyingi zimeelekezwa katika miradi ya maji na ndiyo maana tatizo la maji linaendelea kupungua. Namna ambavyo tatizo lilikuwa huko awali ni tofauti na sasa hivi, na tayari sisi Wizara tunafanya kazi kwa makusudi kabisa usiku na mchana ili kuhakikisha kuona kwamba miradi yote ambayo haitoi maji itatoa maji. Tayari miradi ambayo ilikuwa ya muda mrefu haikuweza kutoa maji. Baadhi tayari inatoa maji na tayari watendaji wetu wanaendelea kufanya kazi. Tutahakikisha miradi yote ambayo maji hayatoki maji yatatoka bombani.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kufuatana na majibu ya Naibu Waziri anasema kwamba mahabusu wana hiari ya kufanya shughuli mbalimbali; kwa sababu mahabusu wengi wanakaa muda mrefu Gerezani; miaka mitatu, nane, wengine mpaka tisa, wengine mpaka 12: Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kupeleka vifaa mbalimbali ambavyo watakuwa wanajiendeleza mle ndani kama ni kushona cherehani; yaani ujuzi mbalimbali wakiwa mle mle ndani, siyo kwenda kufanya kazi nje, kwa kipindi ambacho wanasubiria kesi zao kama zimemalizika wameachiwa huru au kama wamefungwa. Kwa kipindi hiki, kwa nini msipeleke waendeleze ujuzi wao wakiwa mle gerezani? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, Mheshimiwa Hamza Chilo, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mahabusu hawapaswi kufanya kazi kwa mujibu wa Kanuni za Kimataifa na pia sheria za nchi yetu. Hata hivyo, uzoefu unaonesha kwamba katika maeneo ambayo tumepita na kuangalia, wengine wanapenda kufanya zile shughuli za hiari yao kabisa na wanapenda kufanya kazi. Nakubaliana na Mheshimiwa Matiko kwamba katika maeneo ambako tumekuwa na shughuli ambazo haziwaruhusu kutoka nje, kwa sababu mahabusu wanategemeana na aina ya kosa alilolikosa.

Mheshimwia Spika, kwa makosa ya kawaida unaweza kumruhusu hata kutoka kidogo, lakini kwa makosa yale magumu, makubwa, siyo rahisi kumruhusu. Sasa katika maeneo ambayo tumefungua bakeries kwenye maeneo ya Magereza na Shule za Kushona ambazo ziko ndani ya Magereza, kwa kweli wanazifurahia na wanafanya.

Mheshimiwa Spika, tunachukua maoni yake hapa kwamba hicho anachokisema ndicho kinachofanyika hata kwa sasa. Tutajitahidi tu kuongeza uwekezaji kuhakikisha kwamba tunapeleka mashine hizo za kushona au zinazofanana na shughuli za kawaida zinazoweza kufanyika ndani ya Magereza ili waweze kujishughulisha kwa sababu kusema ukweli mtu kukaa bila kufanya shughuli yoyote kwa muda mrefu inakuwa siyo jambo ambalo kibinadamu linakubalika. Hata wao unaona kabisa nimesema nao, wanasema tuleteeni shughuli za kawaida tufanye. Kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ucheleweshaji wa kesi kwa kiasi kikubwa unatokana na upelelezi kutokamilika kwa muda muafaka, na kwa kuwa kuna kesi ambazo, kwa mfano, kuna kesi moja mahabusu amekaa zaidi ya miezi 8, house girl kaiba sijui vitenge viwili kwa mwajiri wake, kesi haikamiliki. Swali langu ninataka kujua; kwa kuwa kesi zinakuwa hazikamiliki, watu wanakaa miaka 8, 10 mpaka 12. Ni kwa nini sasa upelelezi usifanyike ukikamilika sasa, ikifikia hatua ya usikilizaji ndipo watuhumiwa waweze kupelekwa mahakamani, ambapo ndipo itachukua muda watu wasikae magerezani? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa si kila kesi mtuhumiwa anatakiwa kukaa mahabusu, ni baadhi ya kesi ambazo zimetajwa kwa mujibu wa Sheria, kwamba kwa makosa ya aina hii mtuhumiwa hapaswi kuachwa huru. Anatakiwa azuiwe kwa sababu kwanza yeye mwenyewe anaweza akahatarisha maisha yake kutokana na nature ya kosa alilokosa, lakini pili akiwa nje anaweza akaharibu upelelezi, kwa maana ya kesi husika kulingana na hukumu na ukubwa wa kesi yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa ambao wanatuhumiwa kubaki kwa kesi ya vitenge kama anavyosema, hii ni kesi tofauti na pengine ni kesi moja kwa nyingine. Nitoe rai na niseme tu kwamba, kwa yale makosa ambayo, na wewe unafahamu, yanahitaji kabisa dhamana na dhamana ni haki ya mshitakiwa; lakini kwa makusudi tu inazuiwa kutolewa dhamana na sheria inasema kosa hilo linadhaminika; kwamba hiki kitendo hakikubaliki na ni lazima tufuate sheria, sote tuondoe mahabusu kuwa wengi kwa kufanya hivyo. Kwa sababu, kwa kufanya hivyo kutatusaidia sana kupunguza idadi ya mahabusu wengi tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme tu, Serikali hata mara moja, lakini pia hata Idara ya Upelelezi ndani ya Jeshi la Polisi haiwezi hata mara moja ikarefusha upelelezi kwa kesi ambayo inahitaji kumalizwa upelelezi wake. Bali kama kuna jambo limetokea mimi niletewe tushughulikie. Kama kuna kesi ya khanga, kesi ya vitenge, kesi ya bakuli amefanya house girl akakaa miezi minane, ni jambo maalum la kushughulikiwa na nitaomba Mheshimiwa Mbunge tuonane naye ili aweze kunipa taarifa zaidi. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru ni dhahiri kwamba maeneo ya Bugosi na Kinyambi ni tatizo la takriban miaka 17. Mara ya mwisho Serikali kupitia aliyekuwa Waziri wa Ulinzi ambaye ni Rais wa Zanzibar kwa sasa walifanya tathimini kwa mara ya pili hapo mwaka jana na wakawa wameshajiridhisha kwamba ile ya kwanza ilikuwa inawapunja Watanzania wale wa Tarime, na wakasema tayari wameshapitisha wanasubiri HAZINA kulipa hela na aliyekuwa Waziri wa Fedha ambaye ni Makamu wa Rais alidhihirisha hili kwamba tayari Fedha za Tarime zipo tayari kulipwa.

Mheshimiwa Spika, sasa hayo wanayokuja kusema leo inaonyesha ni jinsi gani Serikali haitoi umakini na uzito pale ambapo wananchi wamekuwa wametwaliwa ardhi. Sasa, ningeomba Mheshimiwa Waziri alete zile fedha ambazo zilishapitishwa tayari walikuwa wanasubiria Hazina kutoa ziende kuwalipa wale wananchi wa Tarime ili waende maeneo mengine wapishe jeshi lifanye shughuli zao. Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Spika, niseme tu kwamba ule umakini wa kuhakikisha kwamba wananachi wanapata haki yao ndio huo ambao kwa namna nyingine umesababisha tumechelewa. Pia tumechelewa kwa sababu yapo matatizo kadhaa, Mheshimiwa Matiko anafahamu. Kwamba wakati wa zoezi hili likifanyika kwenye uthamini, na kwa uzoefu umeonyesha maeneo mengi, kumekuwa na changamoto hizi, na hasa Serikali inapoona kwamba kuna wananchi watakosa haki zao.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu sana tukazingatia kwamba wananchi wapate haki zao. ndiyo maana unaona hata uthamini uliochelewa kwa utaratibu wa sheria na kanuni zilizokuwepo kwa nia hiyo hiyo ya kuwa-compensate wananchi kile ambacho wamechelewa kukipata ndiyo maana tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge, vuta Subira; na sisi tumejipanga na sasa tunacho kitengo cha milki kwa nia ya kuhakikisha kwamba kinafanya kazi yake vizuri kwa matatizo hayo. Yako matatizo mengi maeneo mbalimbali; kwamba tumeweka kitengo hiki ili kiweze ku-coordinate ili tuone zile changamoto ambazo zilikuwa zinatokea zinaondoka. Tukienda kwenye hatua ya uhakiki wenzetu upande wa Hazina na kadhalika; changamoto nyingi zimekuwa zikionekana lakini tumedhamiria kuona kwamba maeneo haya,maeneo ya Tarime na maeneo mengine nchini yako mengi tunafanya hivyo kuhakikisha kwamba ile migogoro iliyokuwepo tunaenda kuimaliza. Kwa hiyo Mheshimiwa Matiko naomba uvute subira na ninaamini kwamba tutaenda kulimaliza mapema, tumejipanga vizuri. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nasikitika kwa majibu ya Serikali, bado anarejea mwaka 1997 ilhali swali langu la msingi limerejea mwaka 2016 ambapo Waziri wa Mifugo by then alikuja na Watendaji wa Wizara, wakakaa na Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa Tarime, Rorya na Mkoa wa Mara na tukakubaliana kwa umoja wetu kwamba Mnada wa Kirumi Check Point uendelee na Mnada wa Magena uendelee kwa sababu uko mpakani ili ng’ombe zisipelekwe kuuzwa kwenye Mnada wa Maabel. Maswali yangu mawili ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kama Taifa tunahitaji mapato; na Waziri amekiri kwa mwaka 1996 tu Serikali ilipata maduhuli ya shilingi milioni 260 kwa kuuza ng’ombe 104,000; na huo Mnada wa Check Point tangu mwaka 2014 mpaka leo mmeuza ng’ombe 34,000 tu; ni dhahiri mnada wa mpakani una mapato zaidi: Je, ni lini sasa Serikali itarejea muhtasari wa Kikao ambacho tulifanya mwaka 2016 pamoja na kuambatana na Wizara husika ili twende kwenye Mamlaka ya Mkoa kuhakikisha kwamba Mnada wa Magena unafunguliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Mnada wa Kirumi hauchukui ng’ombe kutoka Serengeti, Rorya wala kutoka Tarime; ng’ombe zinatoka Tarime, Rorya na Serengeti zinaenda Kenya moja kwa moja; na sasa hivi hamna hayo mambo ya usalama, kuibiwa ng’ombe, hayapo kabisa Tarime; mkiendelea kuongea hivi ni kama mnadhihaki wananchi wa kule: Ni lini sasa mtahakikisha kwamba mnajiridhisha hamna wizi wa ng’ombe kutoka Tarime kwenda Kenya au kutoka Tarime kuja huko Kirumi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba, tunakiri tunahitaji sana mapato na Serikali imejielekeza katika kuhakikisha kwamba mifugo na uvuvi inatoa mchango mkubwa katika pato la Taifa. Ni ukweli kwamba Mnada wa Magena uko mpakani na utoroshaji ni mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa rejea yako ya mwaka 2016 iliyofanywa ziara ya Mheshimiwa Waziri wa wakati huo
na viongozi wengine, Wizara ya Mifugo na Uvuvi tuko tayari kuhakikisha kwamba maoni haya uliyoyatoa Mheshimiwa Mbunge tunayachukua na kuendelea kuwasiliana na mamlaka za Mkoa na kufanya rejea na tathmini ili kusudi tuweze kwenda kwa pamoja na kuhakikisha tunaongeza wigo wa mapato sawa na matakwa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Serikali iliahidi kupeleka visima 23 kwenye Halmashauri ya Mji wa Tarime kuweza kupeleka visima hivyo pembezoni mwa kata ambazo zipo nje ya mji tangu mwaka 2018.

Ni lini sasa Serikali itakwenda kuchimba visima hivyo wakati tukisubiria mradi wa Ziwa Victoria?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana dada yangu Mheshimiwa Matiko. Maji hayana mbadala. Maji ni uhai, nasi hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Tarime. Kabla ya mwaka huu wa bajeti kwisha tutafanya shughuli hiyo kuhakikisha wananchi wake tunawachimbia visima vya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mji wa Tarime mpaka leo imesajiliwa kama Hospitali ya Wilaya na kiuhalisia inahudumia wananchi wote wa kutoka Tarime Vijijini kwa huduma za upasuaji, kutoka Rorya, lakini pia watu wengine wanatoka nje ya nchi kwa maana ya kule Kenya tuko mpakani.

Ningetaka kujua ni kwa nini Serikali haijaifanya hospitali hii ili iweze kupata stahiki kama Hospitali ya Wilaya kama vile ilivyo Hospitali ya Kahama Mjini ambayo inahudumia Ushetu na Msalala, kama vile ilivyo Hospitali ya Nzega Mjini ambayo inahudumia Bukene na Nzega Vijijini ili sasa ihudumie sio kwa idadi ya watu wa Tarime Mji bali kwa idadi ya watu halisia wa kutoka Wilaya nzima ya Tarime na wengine kutoka Rorya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kupelekea kupokea watu wengi nje ya Tarime Mji, hospitali ile inaelemewa, haina matabibu wa kutosha, na kama nilivyosema awali wanaleta fedha chache, leo hata ukienda mortuary unakuta ina burst kwa sababu inachukua watu wote kutoka nje.

Ningetaka kujua ni lini Serikali itapanua chumba cha kuhifadhi maiti ili sasa wakati mkibadilisha usajili kuwa wa Wilaya na kuweka stahiki za Wilaya ili mortuary ile iweze kupokea Watanzania ambao wamekutwa wamefariki na kuja kuhifadhiwa pale Tarime Mji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hospitali ya Mji wa Tarime inahudumia pamoja na wananchi wa kutoka katika Halmashauri za jirani na Tarime na ni utaratibu wa kawaida katika hospitali zetu ambazo mara nyingi zipo mipakani, lakini hata zile ambazo zinahudumia wananchi ambao wapo karibu na Halmashauri hiyo.

Kwa hiyo, kuna baadhi ya hospitali za Halmashauri nchini kote ambazo pamoja na wananchi wa ndani wa Halmashauri husika pia zinahudumia wananchi wanaotoka katika Halmashauri nyingine, ni suala la kawaida na utaratibu wetu sisi katika afya hatuna mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitambue kwamba ni kweli tunafahamu hospitali hii inazidiwa na wagonjwa, lakini takwimu zimeonesha kwa wastani kwa siku wagonjwa wanaolazwa ni 70 lakini pia 140 wa OPD. Na Serikali inatambua kwamba tunahitaji kuendelea kuboresha miundombinu katika hospitali hii na sisi tutaendelea kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya watumishi kwa maana ya waganga na wauguzi ili waweze kuendana na mzigo wa hospitali hii. Lakini pia ujenzi wa mortuary ni kipaumbele katika Serikali yetu, lakini pia katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili nilichukue ili twende na sisi tukalifanyie tathmini kuona kwa maana Serikali Kuu na Halmashauri namna gani tutafanya ili tuweze kuondoa adha ya kuwa na mortuary ndogo na kuboresha huduma hizi kwa wananchi. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; ni barabara nyingi sna Tanzania hii unakuta zimeharibika na zinasababisha ajali. Nilitaka kujua mpango mkakati maana yake Waziri amekiri kwamba ni kwa sababu ya malori yenye mizigo mizito yanapita yanasababisha uharibifu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami ambayo itastahimili haya malori ambayo yanakuwa yanapita na mizigo mikubwa na kuharibu barabara na hivyo kusababisha ajali nyingi na kupoteza maisha ya watu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu Serikali ina project ambayo inaendelea ya SGR na vitu vingine. Ni lini itakamilika sasa ili mizigo mingi iweze kusafirishwa kwa njia ya reli na siyo kutegemea barabara ili barabara ziweze kutumika kwa usafiri wa mabasi na magari mengine madogo madogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Kwanza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati wote tunapofanya design ya barabara tunategemea na kiasi cha mizigo itakayopita na ukubwa wa barabara. Lakini kwa sababu ya mabadiliko ya uchumi kumekuwa na mabadiliko makubwa sana ya uchumi ambayo yanapelekea magari ambayo yalikuwa yamepangiwa kupita barabara hiyo hayabadiliki na hivyo lazima tubadilishe design na ndiyo maana tunafanya matengenezo na tunapofanya matengenezo kwenye barabara hizi tunahakikisha tunapofanya matengenezo ambayo sasa magari makubwa na mazito yatapita kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mkakati wa Serikali ni kufanya rehabilitation kubwa kwenye hizi barabara ambazo tunaamini zitachukua magari makubwa na yenye mizigo mizito.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imekuwa ikisimamia na imeendelea kutoa fedha na ni mpango wa Serikali kuanzisha ujenzi wa SGR ili kunusuru barabara zetu na kuhakikisha kwamba mizigo mikubwa sasa badala ya kupita kwenye barabara ipite kwenye reli ya kisasa ambayo SGR na ndiyo maana tayari sasa barabara inaendelea kujengwa na fedha zinaendelea kutolewa ili kupunguza mizigo mikubwa itakayopita kwenye barabara zetu na kunusuru hizo barabara, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; ni barabara nyingi sna Tanzania hii unakuta zimeharibika na zinasababisha ajali. Nilitaka kujua mpango mkakati maana yake Waziri amekiri kwamba ni kwa sababu ya malori yenye mizigo mizito yanapita yanasababisha uharibifu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami ambayo itastahimili haya malori ambayo yanakuwa yanapita na mizigo mikubwa na kuharibu barabara na hivyo kusababisha ajali nyingi na kupoteza maisha ya watu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu Serikali ina project ambayo inaendelea ya SGR na vitu vingine. Ni lini itakamilika sasa ili mizigo mingi iweze kusafirishwa kwa njia ya reli na siyo kutegemea barabara ili barabara ziweze kutumika kwa usafiri wa mabasi na magari mengine madogo madogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Kwanza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati wote tunapofanya design ya barabara tunategemea na kiasi cha mizigo itakayopita na ukubwa wa barabara. Lakini kwa sababu ya mabadiliko ya uchumi kumekuwa na mabadiliko makubwa sana ya uchumi ambayo yanapelekea magari ambayo yalikuwa yamepangiwa kupita barabara hiyo hayabadiliki na hivyo lazima tubadilishe design na ndiyo maana tunafanya matengenezo na tunapofanya matengenezo kwenye barabara hizi tunahakikisha tunapofanya matengenezo ambayo sasa magari makubwa na mazito yatapita kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mkakati wa Serikali ni kufanya rehabilitation kubwa kwenye hizi barabara ambazo tunaamini zitachukua magari makubwa na yenye mizigo mizito.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imekuwa ikisimamia na imeendelea kutoa fedha na ni mpango wa Serikali kuanzisha ujenzi wa SGR ili kunusuru barabara zetu na kuhakikisha kwamba mizigo mikubwa sasa badala ya kupita kwenye barabara ipite kwenye reli ya kisasa ambayo SGR na ndiyo maana tayari sasa barabara inaendelea kujengwa na fedha zinaendelea kutolewa ili kupunguza mizigo mikubwa itakayopita kwenye barabara zetu na kunusuru hizo barabara, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Uwanja wa Ndege wa Musoma ni uwanja wa kimkakati, kwa maana Mkoa wetu wa Mara umejaaliwa madini, mbuga za wanyama, makumbusho ya Baba wa Taifa, samaki na biashara mbalimbali,hivyo ungeweza kunufaisha taifa iwapo ungejengwa kwenye kiwango cha kimataifa ili ndege ziweze kutua moja kwa moja tofauti na ilivyosasa hivi watalii wanatua Nairobi au Arusha ndipo wanakuja kwenye mbuga ya Serengeti.

Ningependa kujua sasa, huu ujenzi na ukarabati ambao unaokadiriwa kukamilika ndani ya miezi 18, unatarajia kuwa na run ways pamoja na jengo la abiria la kiwango cha kimataifa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, pale Tarime tuna Uwanja mdogo wa Magena ambao hutumiwa na watalii na wale ambao wanakwenda migodi kwa kutua na ndege ndogondogo. Na sasa hivi upo chini ya halmashauri ambapo unaikosesha mapato Serikali, kwa maana imekodiswa kwa makampuni binafsi.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kuchukua uwanja ule ili uje kwenye Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kwenye Serikali Kuu ili pia uweze kukarabatiwa na kuweza kutumika na kuongeza kipato cha taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza uwanja wa ndege wa Musoma ni uwanja ambao ni wa kihistoria, ni uwanja ambao uliasisiwa na Baba wa Taifa hili. Vilevile upo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na viongozi wetu wa mkoa wanausimama pamoja na Wabunge wote wa Mkoa wa Mara. Na mimi pia ni sehemu ya eneo hilo la mkoa huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuhakikishie kwamba uwanja tayari, kulikuwa na eneo limebaki, kama mita 105, ili kila aina ya ndege hata kama iwe kubwa iweze kutua pale. Tumeshalipa, fidia imekamilika. Kwa hiyo, ndege zote muhimu zitatua katika eneo hilo na watalii kutoka Kenya watatua Musoma watakwenda Serengeti kwenye shughuli zao, na uchumi wa Mkoa wa Mara na maeneo mengine utafunga.

Vilevile swali lake la pili linalohusu Uwanja wa Ndege mdogo pale Magena. Wiki iliyopita Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi alikuwa pale, amefungua mnada wetu pale wa Magena, maana yake itaongeza soko la kibiashara katika eneo hilo, kuna mifugo itauzwa katika eneo hilo. Uwanja huu upo chini ya Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalipokea wazo hili, tufanye tathmini, tuangalie uwezo wa Serikali, ikiwezekana upanuliwe na kusimamiwa ili ndege ndogo za watalii ziweze kutua pale, na hivyo itapunguza msongamano pia kuja Musoma na badala yake watakuja kule Tarime ambapo kimsingi watalala Tarime, watakula Tarime, watafanya kazi Tarime na uchumi wa Tarime utafunguka. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante; Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni mtu ambaye anaheshimika Tanzania na duniani kote na kwa kufanya hivyo kule Butiama ni sehemu ambayo amezaliwa lakini pia ni sehemu ambayo amezikwa.

Je, ni kwa nini sasa Serikali haioni umuhimu wa kuboresha maeneo yale ya Hayati ili pawe ni historical site ambapo ataelezea kila kitu ili tuweze kupata watalii wengi na kuongeza mapato kama vile ilivyo kwa mwenzetu Hayati Mandela wa Afrika Kusini ambapo watu wengi wanakwenda wanamimika kuweza kujifunza zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali ina maeneo mengi ya kihistoria, lakini tuna eneo muhimu la kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lililoko kule Butiama. Serikali ina mpango wa kuanzisha utalii wa Kiswahili, tuanita Swahili Tourism ambayo kwenye maeneo haya yenye kumbukumbu tutaanzisha Swahili Tourism iwe ni motisha; mtalii anapofika kwenye maeneo hayo basi kwanza atajifunza Kiswahili lakini atasimuliwa historia na kumbukumbu ya waasisi wetu walikuwaje na walifanya nini na ukizingatia kwamba Mwalimu Nyerere alikuwa ni mmojawapo wa waasisi wa kuboresha lugha yetu hii ya Kiswahii.

Nimhakikishie tu Mbunge kwamba eneo hili ni la muhimu na Mbunge wa eneo hilo alishanialika kwenda kule kwa ajili ya kuangalia namna ya kuboresha eneo hili ili liwe chanzo cha mapato ya Serikali. Kwa hiyo, niwatoe wasiwasi Wabunge na hata wale wengine ambao wana maeneo mengine yenye historia kupitia bajeti hii mliyotupitishia tutahakikisha kwamba maeneo haya tunayasimamia kikamilifu ili kuweza kuboresha sekta yetu hii ya utalii, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika nakuskuru. Mradi wa soko la Tarime ulikuwa uanze awali kama alivyosema February 2019 na wananchi wote waliokuwa na vibanda pale takriban 200 walibomolewa vibanda, kwa hiyo wamekuwa wakilipwa kwa muda huu wote, na majibu ya Serikali anasema utamalizika ndani ya miezi 12, na wametenda bilioni tatu tu, wakati mradi ni bilioni 8.07, ninependa kujua sasa hio bilioni 5.07 zinapatikana wapi ili ziweze kumalizika mradi huu ndani ya miezi 12 kama mlivyoonesha, maana yake mwaka wa fedha uko within that?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tuliweza kukidhi tena vigezo vya kupata stendi ya kimkakati ya Galamasara, na wananchi walikuwa wametoa takribani milioni 70 tangu mwaka 2017, ningependa kujua pia stendi hii ya kimkakati ya Galamasara ni lini inaenda kuanza na kumalizika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimwia Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko kwa juhudi zake za kuunga mkono juhudi kubwa za Mbunge wa Jimbo hilo Mheshimiwa Michael Kembaki katika kutetea wananchi wa Tarime Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nimhakikishie kwamba Serikali imeweka mpango wa kuhakikisha miradi mkakati ukiwemo ujenzi wa soko la kisasa katika Mji wa Tarime unakamiliswa, na ndio maana katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 tumetenga bilioni tatu na Serikali itaendelea kutenga fedha hizo kuhakikisha mradi huo unakamilika; pili fedha bilioni 5.07 zitawekwa kwenye mpango ujao wa fedha kuhakikisha linakamilishwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili stand hii ya kimkakati pia ni miongoni mwa mipango ambao Serikali itaendelea kuitekeleza kwa awamu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, lengo la Serikali ni kuhakikisha miradi hii inakamilika na safari ni hatua, tunaanza na hatua moja tunakwenda kukamilisha hatua nyingine, ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa michezo ni afya na kwa sasa dunia nzima ikiwemo Tanzania tunakabiliwa na hili janga la corona na hivyo tunawahamasisha wananchi wetu waweze kufanya mazoezi ikiwepo kushiriki michezo na vifaa vya michezo ni ghali sana. Na kwa kuwa michezo ni ajira kama Taifa tunahitaji kuwekeza kwenye michezo kuanzia kwenye makuzi ya awali ya watoto wetu ili baadaye waje kuwa na vipaji mbalimbali kwenye soka, riadha, basket na mengine; lakini zaidi michezo ni moja ya sekta ambayo inatangaza nchi yetu na kutangaza utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, Serikali haioni kwamba ni vyema sasa iweze kufanya exemption kwa vifaa vyote vya michezo ili viweze kuwa na bei nafuu na watanzania wengi waweze kununua na kujiendeleza kimichezo?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la exemption si jambo ambalo linaweza likatolewa kauli Bungeni, linahitaji mambo mengi ikiwemo uchambuzi wa kina wa kitaalam juu ya faida na hasara zake. Sisemi kwamba vifaa vya michezo havina faida lakini ni jambo ambalo siwezi ukalizungumza hapa. Niseme tu kwamba tumelichukua tuone jinsi gani litakavyokuwa linakidhi mahitaji na vigezo kwa wakati husika basi tutalifanyia kazi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Wananchi wa Bugosi na Kenyambi kule Tarime Mjini walichukuliwa ardhi yao na Jeshi la Wananchi wa Tanzania tangu 2008, na jeshi hili au Serikali ilifanya tathmini mara ya kwanza 2013, 2017 wakafanya tathmini tena, 2019 na mara ya mwisho na ulitilia mkazo hapa Bungeni walikwenda kufanya uhakiki Juni, 2021 na wakatoa namba ya malipo na wakaahidi kwamba kufikia Agosti, 2021 watakuwa wamelipa lakini mpaka sasa hivi hawajawalipa wananchi hawa.

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua ni lini sasa wananchi hawa wa Kenyambi na Bugosi watalipwa fidia zao, ili wapishe Jeshi la Wananchi wa Tanzania waende sehemu zingine kufanya makazi na shughuli za kimaendeleo?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, naomba nimjibu Mheshimiwa Esther Matiko kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika mkakati huo wa miaka mitatu tayari tumeshafanya tathmini na uhakiki katika maeneo yote isipokuwa maeneo ya Zanzibar ambayo ndiyo tutayafanyia quoter hii. Kinachoendelea sasa baada ya huu utathmini ni kufanya uhakiki na uhakiki unaendelea katika maeneo yote ambayo yamefanyiwa tathmini na uhakiki ili tukishakamilisha uhakiki taratibu nyingine zitafuata. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali. Katika kulinda haki za watoto ni lazima au ni sharti tuzingatie wale watoto ambao unakuta hawana kesi, bali mama zao aidha wameenda wakiwa wajawazito au wamekamatwa ni mahabusu au mfungwa akiwa na mtoto ambaye yuko chini ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, katika Gereza la Segerea tumeshuhudia wamama wanakuja na watoto wao pale wa jinsia tofauti, lakini wanachangamana na watu wazima. Kwa hiyo, unakuta mtu mzima labda anataka kwenda kuoga anavua nguo, yuko hivi na mtoto yuko pale. Tunajua kwamba makuzi ya watoto ubongo wao ni kuanzia miezi sifuri mpaka miaka mitano. Kwa hiyo, unakuta unam-affect kisaikolojia.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua sasa, ni hatua gani Serikali inachukua kuhakikisha kwamba wale mahabusu au wafungwa ambao wamekwenda wakiwa wajawazito, wamejifungua wakiwa Magereza au wameenda na watoto wachanga, waweze kutengwa kwenye cell special ya akina mama wenye watoto au wajawazito wasiweze kuchangamana na hawa watu wengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuna hatua nyingi ambazo huwa zinachukuliwa. Huo utaratibu upo na upo tangu zamani. Inawezekana tu labda kuna maeneo yeye ameyashuhudia, ameona kwamba watu wanachanganyika na wengine wanakuwa wanataka labda pengine… kama hivyo. Kikubwa nimwambie kwamba ziko hatua ambazo Serikali inazichukua ikiwemo ya kuwatenganisha ili sasa ikitokea hali kama hiyo, waweze kupatiwa msaada maalum. Ziko hatua nyingi tu ambazo tunazichukua kama Serikali na kama Jeshi la Magereza. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami nitakuwa na maswali mawili ya nyongeza kwanza kwa takwimu tu za Serikali inaonyesha ni kwa jinsi gani ukatili dhidi ya watoto ni mkubwa sana kwenye nchi yetu ya Tanzania ambayo inaenda kinyume na mkataba wa kimataifa ambao tumeingia wa haki za watoto.

Mheshimiwa Spika, takwimu ambayo Serikali imetoa ni za kuanzia januari tu mpaka Septemba, 2021. Sasa asikwambie mtu kama angetoa uanzia za miaka mitatu au minne nyuma inamaana ni janga kubwa sana na hii inaonyesha dhahiri kwamba kuna changamoto ya uratibu ya takwimu maana hapo umetoa sources moja tu kutoka polisi wakati najua kuna sehemu kama Kamati MTAKUWWA, ukienda kwenye ustawi wa jamii, ukienda kwenye mashirika ya siyo ya Kiserikali lakini hata zile familia ambazo zinamalizana juu kwa juu ukikusanya haya matukio mengi takwimu ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ninataka kujua ni utaratibu gani Serikali imeuweka ya kuhakikisha kwamba inatoa takwimu halisia na kwa wakati kutoka kwenye vyanzo vyote hivi ili kuweza kuwasaidia watoto wa Kitanzani kujua ukubwa wa tatizo ni nini kuliko ku-base kwenye polisi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na kusua kusua kutokutenga au tukitenga kupeleka fedha kwenye utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilataka kujua ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wanatenga bajeti ya kutosha na wanaitekeleza kuhakikisha kwamba kuna kuwa na madawati ya kijinsia ya kutosha kuanzia ngazi ya mitaa, wanawawezesha kuwa na Maafisa Ustawi wa Jamii, Kamati ya MTAKUWWA inapata fedha za kutosha ili kutokomeza hii tatizo kubwa la unyanyasaji wa watoto wa Kitanzania ambao wanabakwa, wanalawitiwa, wanauwawa, wanachomwa moto, ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
nimpongeze kwanza Mheshimiwa Naibu Waziri na ninadhani liko suala linalohusu takwimu za unyanyasaji ataendelea kuzijibia.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ninaomba tu nitoe maelezo mafupi kuhusu mkakati huu wa kitaifa wa mapambano dhidi ya unyanyasaji kwa wanawake na watoto kwa sababu Ofisi ya Waziri Mkuu imepewa jukumu la kuratibu na kuziunganisha sekta na utekelezaji wake ukifanywa na Wizara yenye dhamana ya Afya Maendeleo ya Jamii, Wazee, Wanawake na Watoto.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumekuwa na mkakati wa kwanza ambao ulizinduliwa mwaka 2016 mkakati huo wa MTAKUWA na lengo kubwa ilikuwa ni kukidhi matakwa ya kimataifa lakini matakwa ya Taifa vile vile kuhakikisha kwamba tunaweka sawa masuala haya ya unyanyasaji wa wanawake na Watoto na mkakati huo wa kwanza ndiyo unafikia mwisho, unaelekea kufikia mwisho mwaka 2021/2022 tutakuwa tumeumaliza.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni hivi majuzi tu, wiki mbili zilizopita, nilikuwa kwenye kikao cha wataalam kufanya tathmini ni kwa kiasi gani MTAKUWWA I imeweza kufanikiwa. Masuala yaliyoelezwa na Mheshimiwa Mbunge tumeyaona kwamba ni masuala ambayo yameleta utatanishi kidogo kwa namna moja ama nyingine katika utekelezaji wa MTAKUWWA.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo namhakikishia kwamba kwenye mkakati wa pili sasa masuala ya bajeti, masuala ya madawati na ya rasilimali watu katika kuhakikisha MTAKUWWA II inafanikiwa na inafikia malengo ambayo yalikusudiwa yanazingatiwa sasa katika mkakati huu uliopita ambao unafanyiwa tathmini, lakini mkakati utakaokuja haya yote yatazingatiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niwape pongezi sana wenzetu wa Jeshi la Polisi. Wameanzisha madawati mengi ya kutosha katika maeneo mbalimbali kwenye vituo vyao vya polisi kwa ajili ya kusaidia kuhakikisha wanawake na watoto wanapata haki zao. Hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa MTAKUWWA kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutakuja muda ukifika tutaomba ushauri, maoni na hata kwa Waheshimiwa Wabunge ili MTAKUWWA II uweze kufanikiwa kwa kadri ya mpango tuliokusudia kuwaokoa wanawake na watoto dhidi ya unyanyasaji katika nchi yetu. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu ni dogo kweli na fupi. Sote tunakumbuka wakati wa bajeti hapa Mheshimiwa Waziri aliahidi kwamba ile Miji 26 ya Miradi ya (India) itatekelezeka ndani ya muda. Lakini leo wakati Mheshimiwa Mwanyika anauliza kutaka kujua status ambapo tuna mradi huo wa kutoka Rorya kwenda Tarime Mjini. Tunataka kujua exactly ni lini utakamilika huu mradi? Sio kwamba mtuambie mnasubiri kibali kutoka Exim Bank ni lini utakamilika? Maana yake wananchi wanategemea kupata huduma hii ya maji. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na najua dhati ya moyo namna gani wananchi wako wanataka huduma ya maji. Utekelezaji wa miradi ya maji lazima tukubali upitie taratibu ama michakato mbalimbali ambayo inahitajika. Michakato ya manunuzi sisi kama Wizara ya Maji tumekwishaikamilisha. Tunakamilisha taratibu za manunuzi lazima tupeleke katika Exim Bank ambao wanatupa kibali cha (no objection). Sisi kama Wizara ya Maji tumeshazungumza na wahusika kuna mambo machache ambayo wanayakamilisha na muda si mrefu tutapata kibali kile kwa ajili ya kwenda kutekeleza miradi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge Subira yavuta kheri na kheri itapatikana juu ya utekelezaji wa miradi ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime inaelemewa kwa kupokea wagonjwa wengi kutoka nje ya mji wa Tarime mathalani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, Serengeti, Rorya na hata wakati mwingine kutoka nchi jirani ya Kenya.

Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kukamilisha kituo cha afya cha Kenyamanyori pamoja na zahanati ya Nyandoto ambayo imejengwa kwa nguvu za wananchi ili walau kupunguza pressure ambayo inapelekea msongamano katika hospitali ya Mji wa Tarime?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ni kuhakikisha tunajenga zahanati na vituo vya afya ili kupunguza kwanza umbali wa wananchi kupata huduma, lakini pili kupunguza msongamano kwenye hospitali za Wilaya kama ilivyo katika hospitali ya Wilaya ya Tarime.

Kwa hivyo suala hilo ni la msingi na mipango hiyo tayari imewekwa, wito ambao nautoa kwa Halmashauri ya Tarime ni kutoa kufanya tathmini ya mahitaji ya fedha zinazotakiwa kukamilisha kituo cha afya na zahanati, pili kutenga kupitia mapato ya ndani, lakini pia Serikali Kuu tunaendelea kuangalia fursa ya kupeleka fedha ili kukamilisha zahanati hizo, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda kuuliza swali langu la nyongeza kwamba, barabara ya Tarime - Mugumu - Serengeti ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Mara na Tanzania ukizingatia watalii wanaotokea Kenya kuingia Mkoa wa Mara: -

Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ukizingatia wananchi ambao walikuwa wanaishi kandokando ya barabara hii kwa upande wa Tarime wamebomolewa nyumba zao na waliokuwa wanafanya biashara kuondolewa ili kupisha ujenzi wa barabara hii? Je, ni lini ujenzi utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Tarime hadi Mugumu - Serengeti tayari imeshakamilisha usanifu wa kina na Serikali iko kwenye kutafuta fedha kuijenga; lakini ilionekana ni busara kujenga kwanza daraja ambalo lilikuwa linasumbua sana ambalo tumelikamilisha. Baada ya hapo fedha ikishapatikana tutaanza ujenzi kwa kiwango cha lami.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana, vyuo hivi vya VETA ni muhimu sana kwa sababu husaidia katika kukuza ujuzi lakini pia vinaubua ubunifu, na kwa kufanya hivi husaidia vijana aidha kujiajiri au kupata ajira kwa haraka zaidi, asilimia kubwa ya Wilaya za Mkoa wa Mara hazina vyuo vya VETA. Ningependa kujua ni lini Serikali itajenga vyuo vya VETA walau kwa Wilaya ya Tarime, Rorya na Bunda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika Mkoa wa Mara anaozungumza Mheshimiwa Mbunge kwenye maeneo hayo katika Wilaya hizo alizozitaja bado hatujaweza kuzifikia, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika awamu ijayo maeneo ambayo yatapewa kipaumbele ni yale ambayo hatujayafikia hivi sasa kwa karibu.

Kwa hiyo, nimwondoe wasiwasi katika mgawo unaokuja tutahakikisha kwamba maeneo haya aliyoyataja yanapewa kipaumbele na kuanza ujenzi mara moja. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mbuga ya Serengeti ni maarufu sana duniani na watalii wengi sana huvutiwa kuja kutembelea mbuga ile, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali ikiwepo ukosefu wa uwanja wa ndege: -

Mheshimwia Mwenyekiti, kwa kuwa tangu Bunge la Kumi chini ya Mwenyekiti wa Wabunge wa Mkoa wa Mara, Mheshimiwa Wasira, tumekuwa tukifuatilia Serikalini kuhakikisha kwamba ile mbuga ndani ya Serengeti inajengwa uwanja wa kimataifa ili watalii wanaotoka nchi nyingine waje moja kwa moja watue kwenye huo uwanja wa kimataifa wa Serengeti kuliko ilivyo sasa hivi ambapo wanapita Kenya kwa njia za barabara: Ili kuongeza mapato ya nchi, kwa nini Serikali haioni umuhimu sasa wa kujenga uwanja wa Serengeti kuwa uwanja wa Kimataifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge kutoka Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Esther kwa kuendelea kuwa mdau katika Hifadhi ya Serengeti. Tunamshukuru sana kwa sababu ameendelea kutoa mchango mzuri katika Taifa letu ikiwemo Mbuga hii ya Serengeti ambayo imekuwa ikiongoza Kimataifa na duniani kote kama ni Mbuga bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe wasiwasi Mbunge kuhusu suala la ujenzi wa Kiwanja cha Kimataifa cha ndege ambacho Serikali inafikiria kujenga. Suala hili tumepanga kuweka uwanja wa ndege wa Kimataifa kwenye Wilaya ya Mugumu; na tayari Serikali tumeshapeleka maombi ya kuandaa eneo kubwa la uwekezaji, likiwemo eneo la uwanja wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tunalishanya kwa sababu wenzetu majirani tayari wameshaanza mchakato wa ujenzi wa uwanja wa kimataifa na lengo ni kuiua Mbuga ya Serengeti kwa kuleta watalii upande wao, lakini pia iwe rahisi kuingiza Tanzania. Nasi tumeona ni bora sasa tukaingia kwenye ushindani ikiwemo kujenga uwanja huu wa kimataifa ili ndege zinapokuja ziende moja kwa moja kwenye Hifadhi yetu ya Taifa ya Serengeti na moja kwa moja iwe rahisi kuingia kwenye Hifadhi ya Serengeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunafanya hivyo ili kupunguza kelele na miungurumo mbalimbali inayofanyika kwenye uwanja mdogo ule wa Seronera ambao umekuwa ni kero kwa wanyama na hata kiuhifadhi. Hivyo, tunataka kuuhamishia maeneo ya Mugumu ili iwe rahisi kuleta wasafiri/watalii mbalimbali wanaotoka nje ya nchi waje kwa ajili ya kutuletea mapato nchini. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza niseme nasikitishwa na majibu ya Serikali: -

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunafahamu jinsi Taifa letu linavyokumbwa na majanga mbalimbali ya moto, kama kuungua kwa masoko, shhule, nyumba binafsi na hata kwenye biashara mbalimbali kama hoteli na vinginevyo, ambayo inasababisha hasara kwa mali za raia, lakini hata uhai wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, magari ya kisasa, on average, ni kuanzia milioni 500 na kuendelea. Na bajeti ya Serikali imeonesha kutenga bilioni mbili tu kwa maana ya kwamba, watanunua walao magari manne tu tena hayo ni ya wastani. Ni kwanini sasa Serikali isione umuhimu wa kutenga fedha kwa udharura, ili waweze kununua magari walao mawili katika kila halmashauri, kama ambavyo wanafanya kwenye magari ya washawasha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, sote tumeshuhudia wakati wa chaguzi ambazo zinafanyika kila baada ya miaka mitano kwenye majimbo yetu kunakuja magari ya washawasha zaidi ya mawili matatu, ambayo gari moja la washawasha ni takribani milioni 500, kama ilivyo kwa gharama za gari la zimamoto. Je, kipaumbele cha Serikali ni kipi kati ya kulinda mali ya raia na uhai wao dhidi ya kudhibiti wapinzani wakati wa uchaguzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi. Serikali inatenga fedha mwaka huu, imetenga mwaka jana bilioni mbili na nusu, mwaka huu imetenga bilioni mbili. Tutaendelea kutenga fedha hizo au zaidi kutegemea upatikanaji wa fedha ili kuimarisha jeshi hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nikumbushe. Jeshi la Zimamoto na Uokoaji halifanyi kazi peke yake, hushirikisha majeshi mengine na vituo vingine kama viwanja vya ndege, bandari na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, tunathamini mali na wananchi wetu kwa hiyo, mfano anaoutoa wa washawasha hauna uhusiano wa moja kwa moja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.nashukuru sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ni kwa nini Serikali isiweke utaratibu wa kuwawezesha mahabusu au wafungwa kupata fursa ya kuzungumza na familia zao angalau mara moja kila baada ya miezi mitatu, kuliko hivi sasa unaongelea kwenye nondo, unakuta hakuna usikivu wowote ule?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la namna ya kuboresha utaratibu wa kuzungumza aidha wenza wao na familia zao ni jambo ambalo linazungumzika. Kimsingi tukubaliane kwamba sasa hivi utaratibu huo upo, labda Mheshimiwa Esther yeye haridhiki na ile frequency ama muda. Sasa hilo linategemea na mambo mengi, mazingira, kwa sababu masuala ya magereza yanazingatia usalama, kwamba watu walioko ndani na watu wanaokuja, ni lazima mazingira ya magereza iendelee kulindwa kiusalama ili wanaokuja wasihatarishe usalama wa magereza na wafungwa walioko ndani. Ndiyo maana utaratibu huo umewekwa kwa sasa hivi, lakini pale ambapo miundombinu itaruhusu na pengine utaratibu wa kuweza kuwaona mara kwa mara si jambo baya, lakini nadhani ni jambo linalotakiwa kuangaliwa na kutafakariwa kulingana na usalama wa magereza yetu.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Dunia ya sasa ni ya sayansi na teknolojia, hivyo kama Taifa lazima tuwekeze kuhakikisha kwamba tunakuwa na Walimu wa kutosha kwenye masomo haya ya sayansi na hesabu; na kwa kuwa kuna uhaba mkubwa sana wa Walimu waliopo ni takribani asilimia 33 tu. Je, ni nini mkakati madhubuti na wa haraka wa Serikali wa kuhakikisha kwamba inaajiri Walimu wa kutosha ili kukabiliana na changamoto hii?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa wahitimu hawa ambao hawajaajiriwa tangu mwaka 2015 ni takribani asilimia 60 na wengi wao wamekuwa wakijitolea kufundisha bila ajira rasmi. Ni kwa nini Serikali isiwape kipaumbele Walimu hawa wanaojitolea kwa kuwaajiri kwenye maeneo ambayo wanajitolea kwa sasa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholaus Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Matiko kwa ufatiliaji wa karibu wa Walimu wetu wa masomo ya sayansi pamoja na hisabati. Hata hivyo, kama nilivyokwishaeleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali imeendelea kutoa fursa za ajira kwa Walimu hawa, tunajua changamoto ipo na uhitaji upo ni mkubwa. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI yenye dhamana ya kuomba vibali tayari katika mwaka huu wa fedha imeshaomba kibali cha kuajiri Walimu zaidi ya 42,697 ambapo kipaumbele kikubwa sana tutawapa Walimu wa sayansi pamoja na hisabati na wale ambao wanajitolea katika maeneo mbalimbali nchini. Nakushukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; ni kweli kumekuwa na kero kubwa sana kwa hawa wafanyabiashara wadogo wanaokutwa wanafata bidhaa upande wa pili Kenya. Ni kwa nini sasa Serikali isielekeze task force iache huu utaratibu wa kufukuzana na hawa wafanyabiashara wadogo ambapo wakati mwingine inapelekea vifo kwa kuwagonga ili kuwepo na utaratibu wa kiofisi kama mtu amekwepa kodi basi anafatiliwa kuliko wanavyofanya sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan imeshasema na tumeshaelekeza kwamba tuwahudumie wafanyabiashara na hasa tukiwa na lengo la kujenga sekta binafsi yenye nguvu kuhakikisha kwamba wanafanya biashara zao vizuri bila kero. Kwa hiyo, nilichukue hili ili tuone kama kweli shughuli hizo zinafanyika, kero hizo au task force hizo ziweze kukomeshwa mara moja kuhakikisha wanawasaidia badala ya kuwa-harass wafanyabiashara.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ninataka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuboresha vitambulisho hivi vya Taifa ili viweze kubeba taarifa muhimu zote za mhusika?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli baada ya kuanza kutumika kwa Vitambulisho vya Taifa ambavyo vimeonekana vimekuwa na matumizi mengi Zaidi, imeonekana umuhimu wa kuvihuisha vitambulisho hivyo ili vibebe taarifa nyingi na kumpunguzia Mtanzania utaratibu wa kubeba vitambulisho hiki, Leseni na nini. Tunaendelea kuzungumza na wenzetu wa mamlaka nyingine ambazo zina vitambulisho hivyo ili kuweza kuhuisha Kitambulisho hiki cha Taifa kiweze kubeba taarifa hizo kumpunguzia mwananchi kuwa na makadi au vitambulisho vingi. Kwa hiyo, mazungumzo yatakapokamilika Mheshimiwa Esther jambo hilo litafanyika. Ninakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Majibu ya Waziri yameonesha Serikali ina mpango wa kuanzisha Maktaba Mtandao lakini kiuhalisia maeneo mengi nchini hakuna mtandao na umeme. Tunataka kujua ni nini mkakati wa Serikali kushirikiana na Wizara ya Nishati pamoja na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia kuhakikisha kwamba program hii inafika kwa wakati katika shule zetu zote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli anachozungumza Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna changamoto ya mtandao maeneo mengi, lakini nimwondoe hofu kwamba Serikali yetu inaendelea na uimarishaji wa mtandao kwa kujenga mkongo wa Taifa. Nasi kama Wizara tayari tuna mradi mkubwa sana ambao utahakikisha tunakwenda kuziunganisha shule zetu na mkongo huu na vilevile kuziunganisha kwenye mtandao wa internet.

Mheshimiwa Spika, mradi huu utaanza na mikoa 10 katika mwaka huu wa fedha 2022/2023 na tunaamini mpaka kufika mwaka 2025 basi utakuwa umefikia mikoa yote, lakini shule zote zitakuwa zimeunganishwa na mtandao wa internet kuhakikisha kwamba masomo haya ya TEHAMA yanakwenda kufanyika mpaka kule vijijini. Nakushukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru, hospitali ya Mji wa Tarime inahudumia zaidi ya wananchi wa Wilaya tatu na imekuwa ina uhaba wa watumishi wa afya wakiwemo watalaam wa utengamao na mazoezi ya viungo.

Je, ni lini sasa Serikali itatuletea watalaam hawa wa utengemao na mazoezi ya viungo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri, lakini nitamuomba Mheshimiwa Mbunge mimi na yeye tutashirikiana kuangalia kwa maana ya data za Wilaya hiyo na sehemu hizo, kwanza kwasababu amesema hospitali inatumiwa na Wilaya tatu, tutaangalia kuona tatizo lipo wapi.

Moja; kama kuna maeneo ambayo inaweza ikafanyika kwenye Wilaya husika wapelekwe kwenye Wilaya husika, lakini kwenye ajira ambazo zinakwenda kutokea tutaenda kuzingatia kwa kuangalia data za eneo husika na utumishi watakapotuletea kibali hayo yatazingatiwa. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Hospitali ya Mji wa Tarime inakabiliwa na changamoto ya chumba cha kuhifadhi maiti kutokufanya kazi kwa takribani zaidi ya wiki tatu; na ukizingatia Hospitali ya Mji wa Tarime inahudumia zaidi ya Wilaya tatu, kwa maana hiyo, ina maana ina wagonjwa wengi, hivyo inakuwa na maiti nyingi ambazo zinahitajika kupelekwa Kituo cha Afya cha Sirari. Kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Tarime haina fedha za kuweza kukarabati chumba kile cha kuhifadhi maiti, Serikali haiweze kuchukua jambo hili kwa udharura na kupeleka fedha ili kunusuru adha ambayo wanaipata Halmashauri ya Mji wa Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la jengo la kuhifadhia maiti kutofanya kazi katika Hospitali ya Mji wa Tarime, naomba nipokee taarifa hiyo na tutaifanyia kazi kwa haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma hiyo muhimu katika hospitali hiyo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini barabara ya Utegi hadi Kilongwe inayounganisha Nchi za Tanzania na Kenya kwa upande wa Rorya itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tuna kila sababu ya kuunganisha barabara zetu za lami na nchi jirani, lakini tuna barabara za kawaida na barabara kuu. Barabara ambayo tumeunganisha na Kenya ni ile barabara kuu ambayo inatoka Tarime kwenda mpaka wa Kenya ambao tayari ni barabara ya lami. Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa barabara hii inatumika sana na wananchi wa Rorya na Watanzania kupitia Utegi kwenda Rorya, barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kadri Serikali itakapokuwa imefanya usanifu na kupata fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitoa takwimu za upatikanaji wa maji kwenye maeneo yote takribani nchini ambazo hazina uhalisia. Sasa ni lini Serikali itafanya rejea ili iweze kuja na uhalisia wa upatikanaji wa maji kwenye maeneo yetu nchini kuliko ilivyo sasa hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la takwimu, ni suala la pana, pale tunaposoma takwimu 40 percent, maana yake kuna calculation zinazofanyika, zinazojumuisha mtandao wa mabomba, pamoja na namna ambavyo ukubwa wake umefikia katika eneo la usambazaji. Hivyo masuala ya takwimu, katika mifumo ya usambazaji wa maji yanahesabu zake, lakini kikubwa ninachoweza kusema tusiangalie tu hii takwimu, angalieni kazi inayofanywa na Wizara ya Maji, mabadiliko ni makubwa, mageuzi ni makubwa na tutaendelea kuwafikia wananchi wote kutoa huduma safi ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Shule ya Sekondari ya Mogabili ni shule kongwe na ya bweni ambayo inagharamiwa na wazazi na inachukua wanafunzi wengi sana. Imekidhi vigezo ambavyo vimetajwa na Mheshimiwa Naibu Waziri hapa. Nataka tu kujua kama hii shule ya sekondari itapandishwa hadhi kuwa kidato cha tano na sita katika hizo shule 100 ambazo Waziri amezitaja hapa, anatarajia kuzifanya mwaka huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba sio shule zote zimeomba kuwa kidato cha tano na sita. Kwa hiyo nitaangalia katika mpango, kama ipo maana yake tutaiweka katika mipango yetu ili iweze kukamilisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo baada ya kusema maneno hayo naamini Mheshimiwa Mbunge amenielewa.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri amelieleza Bunge lako Tukufu hapa kwamba hamna ucheleweshaji wa kutoa vibali vya kupitisha umeme kwenda vijijini. Sasa nataka kujua, Wizara ya Nishati ilikuja kwenye Kamati ya Bajeti, wakaeleza kwamba moja ya kikwazo kikubwa cha kuchelewesha kupeleka umeme vijijini ni kuzuiwa au kucheleweshwa kwa vibali na TFS. Leo Mheshimiwa Waziri anaeleza kwamba hakuna huo ucheleweshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua katika hizi Wizara mbili ambazo ni za Serikalini, ni yupi anaongea uongo katika kuhakikisha kwamba umeme unafika vijijini kwa wananchi? [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa Matiko hilo neno la uongo naomba uliondoe.

MBUNGE FULANI: Uongo!

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua Wizara ya Nishati na Wizara ya Maliasili na Utalii ni Wizara ambazo ziko ndani ya Serikali...

MWENYEKITI: Imeshaeleweka, ipi ipo sahihi?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naondoa “uongo”, sasa nanyoosha vizuri swali.

MWENYEKITI: Eeeh, ndiyo.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnaliambia nini Bunge na wananchi kinachochelewesha umeme kwenda vijijini wakati nyie ni Wizara mbili ambazo mpo ndani ya Serikali, siyo kwamba ni kutoka hata kwenye sekta binafsi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kusema Wizara zote mbili; ya Nishati na ya Maliasili na Utalii zimesema ukweli. Nataka nimhakikishie tu kwamba Wizara hizi zinafanya kazi kwa ushirikiano. Kabla Wizara ya Nishati haijatekeleza miradi yake, ni lazima mteja awe amekamilisha taratibu zote ikiwemo malipo ya tozo. Kama hajalipa tozo, basi vibali hawezi kuvipata kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niliseme hili wazi kwamba wateja wengi wanasingizia kwamba vibali vinacheleweshwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, lakini ili nikupe kibali, ni lazima uwe umetekeleza masharti yote ikiwemo ulipaji wa tozo. Sasa kama tozo umeshamaliza kulipa, kwa nini mimi nikunyime kibali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndivyo utaratibu unavyotakiwa na wateja wengi wanataka tusamehe ulipaji wa tozo. Kwa hiyo, kama mteja anahitaji kusamehewa tozo, basi awasilishe kwenye mamlaka husika ambayo ni Wizara ya Fedha, na Waziri mwenye dhamana ataangalia kama kuna haja ya kutoa msamaha, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nasikitika kwa majibu ya Serikali, kwa sababu tunatambua kwamba ukatili wa kijinsia umeongezeka, sasa mpaka leo wanatuambia madawati ya kijinsia yako 420 na tuna kata takribani 4000. Ina maana takribani asilimia 10 tu ndio watu wanaopata hii huduma ambao wana athirika. Hata hivyo madawati ambayo wanasema wanatarajia kuanzisha Mashuleni wameanzisha so far, Madawati 1,300 na tuna shule zaidi ya 30,000 kwa Sekondari na Msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kamati hizi anazodai kuamzishwa kwa asilimia 88, aidha hazijaanza kazi labda kwa sababu ya changamoto ya kimuundo au kibajeti. Nataka kujua sasa, ni lini Serikali itazielekeza halmashauri ziweze kutenga bajeti ili kuhakikisha kwamba zinazipatia hizi kamati ambazo zimeanzishwa kwenye hivi vijiji ili ziweze kutekeleza kwa tija na kupunguza au kuzuia kabisa matukio ya ukatili wa kijinsia ambayo yamekithiri katika jamii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa sasa matukio haya ukatili wa kijinsia yanakuwa hayachukuliwi hatua mpaka pale labda vyombo vya habari au mitandao ya kijamii inapo ripoti kwenye jamii ndipo tunaona viongozi wa ngazi za juu wanafuatilia na kuchukua hatua. Nilitaka kujua Serikali imeweka utaratibu upi ambao utawezesha utolewaji wa taarifa na ufuatiliaji wa matukio ambayo yameripotiwa kwenye hizi kamati ambazo mmesema zimeanzishwa kwa asilimia 88 ili kuhakikisha…

MWENYEKITI: Mheshimiwa uliza swalo sasa.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Ndilo swali lenyewe, ili kuhakikisha sasa waathirika wa vitendo vya ukatili wanapata huduma na haki staki kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther ifuatvyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Halmashauri kutenga fedha kwa ajili ya kuimarisha kamati. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Esther kwa wazo zuri ambalo amelitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe waheshimiwa Wabunge ambao wanaingia katika Mabaraza ya Madiwani walipe kipaumbele suala hili ili Kamati hizi ziweze kujiwezesha na baadaye kufanya kazi kwake kwa makini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mifumo na utoaji wa taarifa. Kwa suala hili kwa kuwa utekelezaji wa MTAKUWWA ni mtambuka, Serikali itaendelea kutumia mifumo iliyopo kisheria. Kuhusu swali la Jeshi la polisi ndio muamala ambao unaweza kutoa taarifa za ukatili wakati upelelezi unapo kamailika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Mwananchi aweze kuhukumiwa, Mahakama ndiyo itakayo toa hukumu katika vifungu ambavyo vilivyowekwa. Hata hivyo kesi ili iende haraka tunawaomba waathirika wote wawe na ushirikiano na vyombo vya sheria na pia kuwa wawazi katika kuleta maelekezo yao. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Wilaya ya Tarime haina Chuo cha VETA. Mwaka 2022 niliuliza swali hili hili kwa Mheshimiwa Naibu Waziri na akaahidi kwamba wataiweka kwa upande wa Rorya na Tarime. Nataka nijue, katika hivyo vyuo 63 ambavyo mnatarajia kujenga, Wilaya ya Tarime nayo imo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika kipindi kilichopita Mheshimiwa Mbunge aliuliza hoja hii. Naomba tu Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi hiki cha maswali uje kuangalia orodha iwapo kama Wilaya walioiyoitaja ipo au haipo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa sababu kwa sasa kuna migogoro mingi inayoendelea nchini ambayo inapelekea mpaka mauaji kwenye maeneo ya hifadhi na wananchi;

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kupitia upya sheria za uhifadhi ili ziweze kuendana na nyakati za sasa na kupunguza migongano kati ya wananchi na wahifadhi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto hizi Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati John Pombe Magufuli aliunda Kamati ya Mawaziri nane ambao walipita nchi nzima. Na utekelezaji wake ni kama ambavyo umeona, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imetekeleza kwa kwenda kijiji kwa kijiji, kata kwa kata, wilaya kwa wilaya, kutoa ufafanuzi. Yale maeneo ambayo yameonekana wananchi wanaweza kuachiwa; tumeachia jumla ya vijiji 975 vimerudi kwa wananchi. Kuna yale maeneo ambayo ni ushoroba wa wanyama, ni mahitaji mahsusi kwa ajili ya uhifadhi endelevu yamerudishwa kwa Serikali; na ndiyo maana maeneo ambayo tumeyaachia wananchi walishangilia na tulivyokuwa tunapita wananchi wamefurahi kwamba Serikali imewasikiliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya machache ni kwa ajili ya uhifadhi mahsusi ili kutunza vyanzo vya maji lakini kuhifadhi mazingira pamoja na uhifadhi endelevu, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wakati Naibu Waziri anajibu maswali yake anaonesha jukumu kuu la Serikali pamoja na Serikali za Mitaa ni kujenga, kuhakikisha kwamba viwanja vinajengwa, lakini kuna halmashauri ambazo kwa mwaka mapato ya ndani hayafiki hata shilingi bilioni moja. Hapo ametutajia mfano Halmashauri ya Geita ambayo inapata mrabaha tu shilingi bilioni sita, hao wana uwezo wa kujenga.

Ninataka nijue, ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha zile halmashauri ambazo hazina uwezo zinajengewa viwanja walau vyenye hadhi ya kuhodhi ligi ya mkoa?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naomba nijibu swali moja la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba suala la michezo ni hitaji la wananchi wetu na tunafahamu kwamba vipaumbele vyetu katika nchi ni pamoja na kuhakikisha magonjwa yasiyoambukiza yanaweza kupigwa vita na wananchi wanakuwa salama. Pamoja na kwamba bajeti zetu hazitoshi katika halmashauri, nitoe rai kwa halmashauri zote kutenga fedha hizi kwa kuwa tusipotenga fedha hizi maana yake hatutekelezi sera hii ya maendeleo ya michezo.

Kwa hiyo, hata kama bajeti zetu ni ndogo tutenge, kwa mfano Halmashauri hii ya Masasi, Mheshimiwa Mbunge pia ametenga sehemu ya Mfuko wa Jimbo kuhakikisha ana- support jitihada za halmashauri, kwa hiyo, tuendelee kutenga fedha.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, kwa nini Serikali isiweke kipaumbele ya kununua hayo magari ya zimamoto kwenye mikoa yote ambayo haina pamoja na Wilaya zote nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimejibu katika majibu ya swali la msingi kwamba katika bajeti ya mwaka huu tunaoendelea kutekeleza tutaanza kununua magari ambako mikoa isiyokuwa nayo itapewa kipaumbele baada ya hapo tutaingia kwenye Wilaya, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza naomba ku-register masikitiko yangu kwa majibu waliyoyatoa Serikali.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukishuhudia Serikali inakuwa na miradi ambayo haina mpango mkakati madhubuti ya kuonesha ukomo wa mradi. Mathalani hili Soko la Remagwe limetelekezwa tangu Awamu ya Nne, takribani miaka 10.

Je, ni kwa nini Serikali kwa takribani miaka 10 haikuweza kuwa inatenga walau bajeti kila mwaka ili kuhakikisha kwamba inakamilisha huu mradi ambao inakiri kwamba ni wa kimkakati? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mkoa wa Mara unazalisha mazao ya kibiashara na ya chakula pamoja na mifugo ambapo hulisha ndani ya nchi lakini pia huenda kuuza nchi jirani ya Kenya, ambapo wakulima hawa wanauza kwa bei ‘chee’ baada ya kuwa wameishiwa na muda.

Ni kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa dharura wa kukamilisha soko hili la kimkakati la Kimaitaifa la Remagwe ili kutatua changamoto ya kimasoko kwa wakulima? (Makofi)
NAIBU WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru kwa maswali hayo pia niwashukuru Wabunge wa kutoka Tarime, Mheshimiwa Mwita Waitara na Mheshimiwa Michael Kembaki ambao wamekuwa wakifuatilia sana maendeleo ya ujenzi wa soko hilo. Kama nilivyosema Serikali inajua umuhimu wa masoko haya na ndiyo maana tulianza kujenga katika mipaka yote ambayo ni masoko ya kimkakati. Serikali inaendelea kutafuta fedha kama nilivyosema ilikuwa chini ya ufadhili wa benki, ufadhili huo uliisha, kwa hiyo tunatafuta fedha nyingine zaidi ili tukamilishe kujenga majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, zaidi tumeshawaambia wenzetu katika Halmashauri kuanza kutenga fedha kidogo kidogo katika bajeti zao kutokana na umuhimu wa masoko haya, kwa hiyo wanachokisema ndiyo Serikali inachokifanya na tunaendelea kufanya hivyo lakini kwasababu ni masoko ya kimkakati yana miundombinu muhimu, kwa hiyo ni lazima tupate fedha za kutosha ili tunapokuja kurudia sasa tukamilishe kwa pamoja kuhakikisha masoko haya yanakamilika katika viwango vinayotakiwa. Nakushukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mji wa Tarime ilipaswa upate maji kutoka Ziwa Victoria kwenye mradi wa miji 21 na Waziri wakati wa bajeti iliyopita aliahidi hapa kwamba kufikia Septemba utakuwa huo mradi umeshaanza na kuelekea matumaini ya kumalizika, lakini mpaka sasa hivi bado haujaanza. Sasa, ni lini huu mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda mji wa Tarime utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni miji 28 siyo miji 21. Miji 28 itaanza kutekelezwa hivi punde kabla ya mwaka huu wa fedha kuisha.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; barabara ya Singida – Iguguno – Mkarama – Sibiti – Meatu imejengwa kilometa 25 tu, na sote tunafahamu barabara hii ni shortcut kwa watumiaji au wasafirishaji wanaokwenda Mikoa ya Mara na Simiyu.

Sasa ni kwa nini Serikali isitafute fedha kwa udharura wake kuhakikisha kwamba hii barabara inakamilika ile sehemu iliyobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu na ni njia fupi sana, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imejipanga na inaendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba barabara hii sasa tunaijenga na kuikamilisha. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kwanini sasa Serikali haina mikakati ya kuhakikisha kwamba halmashauri zenye vyanzo vidogo vya mapato iweze kuwa inawapa fedha nyingi kuliko ambazo zinatengwa ukilinganisha na halmashauri nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwanini Serikali isitumie vigezo vya ukubwa wa eneo ili kuhakikisha kwamba inatoa fedha kulingana na kipaumbele, kulingana na ukubwa wa eneo husika, kuliko wanavyofanya sasa hivi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na vyanzo ambavyo halmashauri wanakusanya kwa mapato ya ndani vinatofautiana kati ya halmashauri moja na nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hoja ya Mheshimiwa Mbunge, kwamba zile halmashauri zinazopata mapato kidogo ya ndani zipewe fedha zaidi. Ni kwamba suala hili linakwenda kuzingatia pia mara nyingi, ukiziona halmashauri hizi zenye mapato madogo ni halmashauri pia ambazo zina population ndogo lakini pia zina shughuli za kibiashara ndogo zaidi ukilinganisha na halmashauri zenye mapato makubwa kwa sababu mapato yanatokana na shughuli za kiuchumi katika halmashauri husika.

Kwa hiyo, utaratibu wa kupeleka fedha unazingatia pia population ya eneo husika, lakini pia na shughuli zile, kwa mfano miradi ya kimkakati ambayo ilitakiwa kwenye kuwekezwa kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tutaendelea kufanya tathmini kuona uwezekano wa kuongeza zaidi package za maendeleo kwa halmashauri zenye mapato madogo, ukilinganisha na halmashauri zenye mapato makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kuzingatia ukubwa wa eneo la kijiografia, suala hili linategemeana na ukubwa lakini pia population kwa sababu fedha za maendeleo zinapelekwa kwa ajili ya kusaidia wananchi. Kuna halmashauri ambazo ni kubwa sana zina maeneo ya hifadhi za misitu na kadhali. Kwa hiyo, ukiangalia tu ukubwa wa jiografia utapeleka fedha nyingi eneo ambalo lina population ndogo kwa sababu tu kuna ukubwa wa jiografia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunazingatia yote, ukubwa, population lakini pia na shughuli zingine za kimaendeleo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushuru. Kuna utafiti ulifanywa na Jumuiya ya Viongozi wa Dini kuhusiana na mambo ya Bima ambao unaonyesha takribani Watanzania milioni 15 hawana uwezo wa kabisa wa kujikatia hii Bima ya Afya.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuweza kuwakatia hawa Watanzania Milioni 15 waweze kupata matibabu wakati huo wakisubiria Bima ya Afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali zuri la Mbunge. Kwanza, moja kupanga ni kuchagua na tunaopitisha bajeti ni sisi, kwa hiyo kikubwa tayari Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa sababu imejulikana kweli kwamba kuna asilimia 28 ya watu ambao hawawezi kujilipia, Rais wetu ameshakubali itengwe kila mwaka bilioni 149.77 kwa ajili ya kuwahudumia watu hao ambao unasema.

Mheshimiwa Spika, wakati tunapanga nikuambie tu ni rahisi sana kungojea wewe LUKU iingie kwenye nyumba ukaacha kuwa na giza lakini ukiugua haisubiri. Kikubwa tunachowaambia wakati wa kupanga na kuamua vipaumbele tukate kodi wapi hasa kwenye Bima ni wakati wa sisi Wabunge kuchagua tunaelekea upande gani.

Mheshimiwa Spika, ahsanteni sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Uhalisia wa upatikanaji wa mbolea kwa wakti kwa wakulima wetu bado ni changamoto kubwa; na inasemekena mbolea hizi zinatumika kusafishia madini kwenye migodi. Sasa nilitaka kujua, ni Serikali itafanya tafiti za kina kujua matumizi ya ziada ya mbolea hizi nje ya kilimo ili kuweza kuwa na bajeti halisia ya kuwafikia wakulima kwa wakati kulimo ilivyo hivi sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya msingi ya mbolea yanafahamika, ni kwa ajili ya kilimo. Kama kuna jambo lingine la ziada kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema, sisi na wenzetu wa madini tutakaa tushirikiane ili kuweza kulifanyia utafiti wa kina na kuweza kupata majibu stahiki katika eneo hili ili mwisho wa siku tuwe na mbolea kwa mahitaji halisi yanayohitajika katika kilimo chetu cha msingi Tanzania. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, barabara inayoanzia Wilaya ya Rorya inapita Susuni – Sirari – Mbogi – Nyansincha mpaka Nyanungu ni barabara ya kiusalama ambayo iko mpakani.

Nilitaka kujua barabara hii ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami ili kuweza kuimarisha usalama katika mpaka wa Tanzania na Kenya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri barabara hii kabla ya kuja Bungeni nimeipitia yote, na ikiwa ina mahitaji makubwa sana pia ya Mkoa wa Mara kwa maana ya usalama. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaifanyia kazi kuhakikisha kwamba hii barabara inaimarishwa na kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru na nasikitishwa kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mgodi wa North Mara walifanya tathmini pamoja na kubomoa nyumba na mazao ya wananchi mwaka 2013, ambapo walifanya tathmini kwa phase sita, baadae baada ya miaka kadhaa wakaja wakasema wanahitaji phase nne tu ambazo wamelipa zikabaki phase mbili zenye wananchi 1,586 na wakasema kama walivyosema kwamba wangelipa kifuta jasho ambapo mpaka sasa hivi wananchi hawa hawajaweza kulipwa kifuta jasho takribani miaka kumi, ningependa kujua ni lini Serikali itahakikisha inasimamia sheria zile za madini na za ardhi kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanalipwa fidia yao stahiki ya kubomolewa nyumba, mazao na muda uliopotea kutofanya shughuli za maendeleo kwa muda wa miaka kumi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, mwaka 2018 baada ya wananchi hao kuona kwamba inachukua muda hawalipwi hicho kifuta jasho kinachosemwa waliifungua kesi Mahakama Kuu, ambapo Waziri wa Madini Mheshimiwa Biteko alienda kule Nyamongo akawasihi wananchi waondoe hii kesi mahakamani mwaka 2018 lakini mpaka sasa hivi wananchi hao bado hawajaweza kulipwa. Mwaka huu mapema walifuatilia kwa Mthamini Mkuu wa Serikali na akakiri kwamba hajapokea document yoyote ile au taarifa yoyote ile ya kutoka mgodini kuhakikisha kwamba wananchi wanaweza kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kujua ni kwa nini pale ambapo mgodi au ardhi ya wananchi inatwaliwa Serikali inashindwa kufuata sheria zilizopo kuhakikisha kwamba wananchi wanalipwa stahiki zao mara moja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili madogo ya Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatanyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali lake la kwanza kwamba ni lini hawa wananchi wanaokaa katika Phase Mbili zilizobaki ambazo hazijafidiwa watalipwa. Napende tu kumhakikishia kwamba baada ya kampeni kumwajiri Mkandarasi aliyefanya tathmini kufahamu watu wanostahili kulipwa na kufahamu kiwango ambacho kinastahili kutolewa kama kifutajasho kwa sasa hivi ndani ya miezi miwili ijayo utaratibu wa malipo hayo utaenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali lake la pili, kwamba ni kwa nini Serikali isisimamie sheria yake na kuhakikisha kwamba wananchi ambao waliondoa kesi Mahakamani mwaka 2018 wanalipwa, napenda tu kumhakikishia kwamba Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan ni Serikali inayopenda kutenda haki, nasi kama Wizara kwa niaba yake tunasimama kidete kuhakikisha kwamba wananchi hawa baada ya hizi tathmini kuwa zimeshafanyika na sasa tumeshafikia mwisho wake na wanakwenda kupata malipo yao, ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuweza kuongezea katika majibu mazuri ambayo ameyatoa Naibu Waziri wa Madini. Nilitaka kuzungumzia suala la fidia kwa nini fidia zinachelewa kulipwa na kwa nini pengine hali inatokea namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la fidia ucheleweshaji wa fidia wakati mwingine unatokana na udanganyifu unaokuwepo kwenye maeneo husika. Kwa mfano, katika masuala mazima ya kuwa na tuna lugha rahisi inaitwa tegesha, unakuta mazao yanaota kwa haraka kwa siku mbili mazao yapo ambayo yanakuwa ni pandikizi kwa hiyo katika suala zima la kufanya uthamini kadri unavyokwenda unakuta kuna mabadiliko kwenye lile eneo, lakini wanasahau kwamba Serikali huwa inachukua picha za anga kabla ya kufanya zoezi na inaangalia picha za nyuma na kuweza kujua kabla ya uthamini kuanza kulikuwa na nini pale na unapoanza uthamini unakuta kuna mali nyingi zinaongezeka, upandaji wa mazao ambayo mengine yanapandwa usiku na mchana. Kwa hiyo, wakati mwingine niwaombe tu wananchi ya kwamba Serikali ina nia na dhamira njema ya kuweza kulipa fidia, kwa hiyo tuache ule udanganyifu ambao unachelewesha haki za Watanzania katika kulipwa fidia zao.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Taasisi ambazo zinaongoza kudaiwa deni na TANESCO ni Taasisi za Serikali tena zile andamizi, za binafsi either hamna kabisa au ni moja, mbili au tatu, nataka kujua sasa kwa sababu kuna Taasisi zingine zinatoa huduma kwa wananchi, haziwezi kukatiwa umeme. Je, ni kwa nini Serikali isiweke pre- paid meter kwa hizi Taasisi zote ili ziweze kuwajibika na kuona kipaumbele cha kwanza cha ku–fine kuweza kulipia umeme kuliko hivi sasa kuweza kuleta usawa kati ya wananchi na hizi Taasisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii bilioni 244 Serikali inadaiwa kama bilioni 86 hivi kwa hiyo bilioni mia moja ishirini na kitu zinazobakia wateja binafsi na watu mbalimbali ndiyo wanaodaiwa. Hao wateja binafsi ni wale wateja wadogo wadogo na kama nilivyotangulia kusema, madeni haya hasa ni ya kipindi kile ambapo hatukuwa na meter.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa utaratibu tunaokwenda nao tumeshaongea na wenzetu Serikalini kukubaliana kwamba pesa inayolipwa kwenye zile taasisi kwa ajili ya kulipia huduma ya umeme, hii ya deni ikatwe at source kwa maana ya kutoka Hazina, lakini hizi pesa nyingine zinazokuja basi tuweke utaratibu mzuri ambazo tutaweza kuzikusanya. Pre paid meters na na hizo smart meters zinazokuja tutahakikisha tunazi–roll kwenye maeneo yote ili kila mmoja aweze kuwa na wajibu wa kulipa deni lake kwa wakati tukihakikisha kwamba sasa ni kwa manufaa yetu sisi wazalishaji na watumiaji wa umeme tunaozalisha.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hali ya hewa ya Tarime na ardhi vinaruhusu kilimo cha zao la chai. Miaka ya nyuma wananchi walikuwa wakilima chai, lakini waliacha kutokana na kutokuwepo na masoko na bei kuwa chini. Sasa kwa mikakati ambayo Serikali imeainisha hapa, nataka kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inahamasisha na kufufua zai la chai kwa Wilaya ya Tarime ili kuweza kukuza uchumi wa wana Tarime? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Tarime ilikuwa ni eneo mojawapo la uzalishaji wa chai na wananchi waliacha. Siyo Tarime tu, hata Mkoa wa Kagera na wenyewe ulikuwa ni eneo mojawapo la uzalishaji wa chai, na Serikali ilibinafsisha baadhi ya maeneo ambayo wawekezaji waliopewa maeneo yale walishindwa kuyaendeleza. Kwa hiyo, kama Serikali sasa hivi, kwa mfano, maeneo ya Kagera tumeanza maongezi na mwekezaji aliyeshindwa ili tuweze ku-take over kile kiwanda kupitia ushirika na Serikali kuweza ku-bail out tuweze kufufua chai eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutafanya tathmini economically, kuangalia kama tuendelee na jitihada tunazozifanya kwenye mazao ya chakula na mazao ya kahawa kwenye eneo la Tarime, ama tulilete zao la chai na litatuathiri namna gani? Kwa hiyo, naomba nitumie nafasi hii kumhakikishia Mbunge tutafanya tathmini and then tutakuwa na majibu ya uhakika. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wananchi wa kata ya Kenyamanyoli waliamua kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao wenyewe, kwa maana Kituo cha Afya cha Kenyamanyoli, lakini Serikali iliahidi kupeleka fedha kuanzia mwaka 2019 kwa ajili ya umaliziaji wa maboma yale, mpaka leo hawajapeleka. Ningetaka kujua ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa yale maboma ili wananchi wa Kenyamanyole waweze kupata huduma ya afya?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha inaunga mkono jitihada za wananchi popote pale nchini ambapo wamejitoa kujenga huduma mbalimbali wao wenyewe kwenye jamii yao; na Serikali itatafuta fedha kadri ya upatikanaji wake ili iweze Kwenda kuunga mkono hujudi hizo katika Kituo hiki cha Afya cha Kenyamanyoli. Vilevile nichukue nafasi hii kumuelekeza Mkuruhenzi wa kule Tarime Mjini, kuhakikisha anatenga fedha kwenye mapato yake ya ndani kuunga mkono jitihada hizi za wananchi wa Kenyamanyoli.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Baada ya wananchi kunyang’anywa ile ardhi, wananchi wa Nkongore mwaka 2020 kabla ya uchaguzi walikuja hapa Dodoma kumwona Waziri Mkuu na Waziri Mkuu aliahidi kwamba, wataenda kurudishiwa lile eneo. Sasa mpaka leo bado hawajarudishiwa na mbaya zaidi hao magereza ambao wamekabidhiwa kwa ajili ya ulinzi kuna shughuli tena wanafanya. Nataka kujua ni kwa nini sasa pale ambapo Serikali imeamua kutwaa ardhi kwa ajili ya matumizi mbadala isiwalipe fidia wananchi? Ni nini taarifa ya fidia ya wananchi wa Nkongore ili waweze kupata kifuta jasho waendelee na shughuli zao ambazo walikuwa wakifanya Serikali inachukua ile ardhi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali pili. Mheshimiwa Waziri ameeleza hapa kwamba, imesababisha kwa sababu ya taratibu za kimazingira wakakabidhi Jeshi la Magereza, ulinzi na usalama, lakini wananchi wale wakati ardhi inachukuliwa walikuwa wamepanda miti ya kudumu pamoja na mazao mbalimbali. Sasa mbaya zaidi askari magereza hawa wanavuna ile miti ya kudumu ya wananchi, wanaenda kufanyia shughuli nyingine. Ni kwa nini sasa kama ile miti inaruhusiwa kuvunwa nje ya hizo taratibu ambazo amezitaja hapa, wasiruhusu wananchi wale wavune miti yao ambayo walikuwa wameipanda kwa ajili ya biashara ili waweze kupata fedha zao stahiki?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hili la wananchi kuwalipa fiidia ya maeneo yanayotwaliwa kwa mujibu wa sheria, nimeeleza kwenye jibu la msingi kama Mheshimiwa Mbunge amenisikiliza kwa makini kwamba, maeneo ya milima ni maeneo yanayohifadhiwa. Hakuna mtu anayeweza akadai kwamba, anamiliki mlima, kwa hivyo, kama walikuwa wanafanya shughuli za kibinadamu kando mwa milima ambazo sio sehemu ya mlima tutawasiliana na mamlaka husika, kwa maana ya Mji wa Tarime. Namwomba Mheshimiwa Esther Matiko tukutane baada ya kipindi cha maswali na majibu ili anipe ufafanuzi mzuri, niweze kutoa maelekezo stahiki kwa wenzetu w akule Tarime.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwepo wa miti iliyokuwa imepandwa na wananchi. Kama kuna uthibitisho huo tutawasiliana na mamlaka husika, kwa maana ya Magereza Mara na Tarime, Rorya, ili waweze kuwaruhusu wananchi wakate miti yao, lakini tunachoshukuru ni kwamba, hata Jeshi la Magereza katika hali ya kutunza ile hifadhi ya mlima wameshaanza kupanda miti na sasa wamepanda karibu miti 1,000 kuzunguka ule mlima kama sehemu ya kuhifadhi mazingira yale, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kulingana na fursa mbalimbali ambazo Mheshimiwa Waziri ameziainisha hapa zimepelekea kuwepo kwa wimbi kubwa la wawekezaji kutaka kuja kuwekeza nchini. Sasa nilitaka kujua, je, Serikali inatumia vigezo vipi kuweza kuwatambua wawekezaji wenye tija kwa Taifa hili? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Nchi yetu kwa sasa inapokea idadi kubwa ya wawekezaji na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mazingira mazuri ambayo anayaweka katika kuvutia wawekezaji. Lakini tunavyo vigezo maalum vingi vya kuweza kutambua ni mwekezaji gani tumpokee na tumpeleke wapi. Naomba nitaje vitano tu;

(i) Tunahakikisha kwamba tunapokea uwekezaji ambao hatimaye utasababisha kukidhi mahitaji ya bidhaa za ndani;

(ii) Tunapendelea sana uwekezaji ambao hatimaye utaongeza thamani ili kuhakikisha kwamba tunaongeza thamani ya vitu vyetu ikiwepo kwenye thamani ya mazao;

(iii) Tunaangalia uwekezaji ambao hatimaye utazalisha ajira kwa watu wetu. (Makofi)

(iv) Tunazingatia sana uwekezaji ambao utatusaidia kuongeza mauzo ya bidhaa nje ya nchi ili kuongeza fedha za kigeni na;

(v) Tunazingatia sana uwekezaji ambao utadhalisha utajiri kwa watu wetu kwa hivyo kuchochea uwekezaji ndani.

Mheshimiwa Spika, hayo ni baadhi ya vigezo ambavyo tunazingatia.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nataka kujua Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuhakikisha kwamba inajenga vituo vya polisi vyenye hadhi ya kipolisi kwa Wilaya ya Tarime, Sirali, Nyamwaga na Utegi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli na Mheshimiwa Mbunge anatambua kwamba Mkoa wa Tarime – Rorya ni mkoa wa kipolisi, lakini kiutawala wako chini ya Mkuu wa Mkoa mmoja. Hata hivyo, tumeanza kutekeleza mpango wa ujenzi wa maeneo haya mapya. Ninatambua kwamba Jengo la RPC Tarime – Rorya almost limekamilika na sasa, tunakwenda kwenye ngazi ya Wilaya ili kujenga vituo vya ngazi ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa mujibu wa mpango wetu vituo vya Wilaya kwenye Wilaya mpya za kipolisi viko mbioni kwa mujibu wa utekelezaji wa mpango wetu wa miaka kumi. Nyamwaga na Sirali ni sehemu ya vituo vitakavyojengwa, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kumekuwepo na kukatwa kwa kodi za majengo kwa wale ambao hawastahilin kukwatwa kwa mfano, wazee na zile nyumba za tembe. Sasa, ninataka kujua ni lini Serikali itafanya reconciliation ili iweze kuwarudishia gharama zote ambazo wamekatwa hawa ambao hawastahili kukatwa kodi hizi za majengo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema na kama tulivyosema kwenye budget speech ya juzi, wenzetu wa Wizara ya Fedha wameshalichukua nasi tulichowa-supply ni namba za LUKU kwa ajili ya wao kuwa-identified nani anastahili kulipa kiasi gani na kwa wakati gani na kwa utaratibu gani. Tunashirikiana nao wenzetu ili waweze kuweka utaratibu mzuri ambao utahakikisha yule anayetakiwa kulipa kweli ndiye anayelipa kama tulivyosema juzi kiwanja kimoja kinaweza kuwa kina vyumba vitano, sita halafu kila mmoja analipa wakati hakutakiwa kulipa kilo mmoja, lakini tunafahamu pia sheria nyingi zinaeleza kwamba wale wazee wa miaka 60 na zaidi wawe-exempted kwenye hayo maeneo na wastaafu wengine tumeshawasiliana na wenzetu na tunalifanyia kazi naamini wenzetu wa Wizara ya Fedha watakamilisha na tutafikia sehemu nzuri.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za pembezoni katika Halmashauri wa Mji wa Tarime ni pamoja ya Kata ya Nyandoto na Kata ya Kenyamanyori. Wananchi wa Kata ya Kenyamanyori walishaanza kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao wenyewe na baadhi ya maboma yamekamilika kuanzia mwaka 2019, Serikali iliahidi kwamba itapeleka fedha kuhakikisha kwamba kituo kile kinakamilika maana wako nje ya mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kujua commitment ya Serikali sasa ni lini watapeleka fedha ili waweze kukamilisha Kituo cha Afya cha Kenyamanyori kupunguza adha ambayo wanaipata kuja kupata huduma kwenye hospitali ya Mji wa Tarime?

Swali langu la pili, katika Kata za Susuni na Mwema katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime ni Kata ambazo zipo pembezoni na wanapata huduma sana sana wakienda kituo cha Sirari kule au hospitali ya Nyamwaga lakini wengi wanakuja Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime. Ninataka kujua ni lini Serikali itahakikisha kwamba Kata hii ya Susuni na Kata ya Mwema na zenyewe zinapata vituo vya afya ili kuweza kupunguza adha ya wananchi wale kusafiri mwendo mrefu kutafuta huduma ya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Esther Matiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kwanza la lini fedha itakwenda kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya Kenyamanyori.

Kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Kata ya Kenyamanyori kwa kuweza kuanza kwa jitihada zao wenyewe ujenzi wa kituo chao cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la fedha tutatuma timu pale ya Mganga Mkuu wa Mkoa kwa ajiili ya kufanya tathmini ya ujenzi ule ambao umefanyika na kuona kama vinakidhi mahitaji yanayotakiwa ili kusajili kituo cha afya kipya katika Kata ile na baada ya tathmini ile wataiwasilisha Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatafuta fedha ya kupeleka kuunga mkono juhudi hizi za wananchi wa Kenyamanyori kumalizia kituo kile cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Kata ya Susuni na Mwema zilizoko kule Halmashauri ya Wilaya ya Tarime. Tutafanya vivyo hivyo kama ambavyo nimemjibu swali lake la kwanza la kuhakikisha timu ile inapoenda Tarime Mji, wafike vilevile kwenye Halmashauri ya Wilaya Tarime na kufanya tathmini katika Kata hizi mbili ambazo amezitaja Mheshimiwa Matiko na kisha walete taarifa Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili tuweke katika mipango yetu ya kutafuta fedha na kuhakikisha kwamba tunapeleka kwa ajili ya kujenga vituo hivi vya afya.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ni lini mtahakikisha mnaondoa askari polisi kujihusisha na ukusanyaji wa kodi kwenye mipaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni lini tutaondoa askari polisi? Askari polisi ni chombo cha usalama, usalama wa mali na usalama wa wananchi. Hatuwezi kuwaondoa sehemu za mipakani, kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutafuatilia nini kinatokea huko katika biashara hiyo ya mipakani. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wanyama wakali wakiwadhuru binadamu kwa maana ya wakivunjika, wakapata ulemavu wanalipwa kifuta jasho cha shilingi 500,000 na wakiuwawa wanalipwa shilingi 1,000,000; wakiharibu mazao ekari moja shilingi 25,000.

Sasa ni kwa nini Serikali isi-review kanuni zao ili ije na uhalisia wa kuweza kutoa kifuta jasho ambacho kinakidhi ustahiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa kuwa hivi vitendo vya ukatili wa kijinsia vimekuwa vikiongezeka nchini, na tumetambua huo mkakati wa Serikali kuhakikisha vituo na kuajiri ustawi wa jamii, lakini nataka nijue sasa mkakati kabisa wa kuhakikisha kwamba tunaondoa kabisa huu ukatili wa kijinsia. Mkakati gani ambao Serikali inao kuhakikisha kwamba, yani kunakuwa na zero ukatili wa kijinsia Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, natambua kuwa kuna vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya wanawake na watoto hapa nchini. Jukumu letu ni kuhakikisha wanawake na watoto wanaofanyiwa vitendo hivyo vya ukatili kuwapatia huduma muhimu ikiwemo ushauri nasaha ili wasiathirike kiakili pale wanapopata vitendo vya ukatili, ahsante. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri kuhakikisha jamii nzima inashirikiana katika jambo hili la kutokomeza ukatili wa watoto, wanawake na makundi maalum nchini, lakini nadhani Bunge lako tukufu linafahamu kwamba Serikali inao mpango mkakati wa kitaifa wa kutokomeza unyanyasaji wa makundi haya maalum ambao ni jumuishi kwa sekta zote, na kila Wizara imeshirikishwa katika kuhakikisha mkakati huo maarufu kwa MTAKUWA unafanikiwa na unazaa matunda ya kuhakikisha Taifa hili la Tanzania linakuwa mstari wa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo tumeshuhudia Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan yeye mwenyewe kwa kuzingatia matakwa ya kimataifa amekuwa mstari wa mbele kutengeneza afua ambazo zitasaidia mapambano hayo dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia katika Taifa letu. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Vituo vya Polisi vidogo yaani kwamaana ya outpost nyingi zimechakaa sana zina hali mbaya nyingi zinavuja mapaa mbao zimeoza yaani hata hao mapolisi wanaofanyakazi huko vijijini Mungu anawalinda. Ningetaka kujua ni lini sasa Serikali itakarabati vituo hivi vidogo vyote Tanzania nzima ili viweze kuwa na hadhi ambavyo vinafaa kuwahudumia wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua na nimesema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba tunatambua uwepo wa uchakavu kwa baadhi ya vituo vya polisi vikiwemo hivi vituo vidogo. Katika mkakati wetu wa ujenzi na ukarabati wa maeneo haya tutazingatia pia hivi vituo vidogo vya polisi kama ambavyo tumeanza kufanya kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Gereza la Tarime limejengwa tangu mwaka 1942. Miundombinu imechakaa ya maji safi na maji taka. Na kwa kuwa wakati Naibu Waziri anajibu hapa amesema hawategemei vyanzo vya ndani na Gereza la Tarime hatuna vyanzo vya ndani. Ningependa kujua mango Madhubuti wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wanakarabati miundombinu ya maji safi na taka ili wale watu waweze huduma hii bila matatizo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba magereza mengi likiwemo hili Gereza la Tarime limejengwa siku nyingi na ni moja ya magereza yaliyochakaa. Kama nilivyokwishasema katika jibu letu la msingi kulingana na upatikanaji wa fedha gereza hili pia litapewa kipaumbele angalau katika bajeti za miaka miwili ijayo, ahhsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kumekuwepo na mwingiliano mkubwa wa mawasiliano na minara ya Safaricom kwenye kata ambazo ziko mpakani kwa upande wa Tarime na Rorya. Na hii inapelekea gharama kubwa kwa watumiaji kwa maana inaingia kwenye roming lakini pia uhafifu wa mawasiliano. Sasa nilitaka kujua ni lini Serikali itahakikisha inapeleka minara toshelezi ili wananchi wa kule waweze kupata mawasiliano bila kuingia upande wa Kenya wanakuwa kama wako Kimataifa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge wa Viti Maalum Kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa katika maeneo ya Wilaya ya Rorya pamoja na Tarime kuna changamoto ya mawasiliano na changamoto yenyewe ni kuingiliana. Vilevile Serikali kupitia mradi wetu wa special zone and boarders tayari maeneo hayo tumeyazingatia kuhakikisha kwamba mawasiliano yanaenda kuimarishwa ili kusiwepo na mwingiliano wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tunaelewa kabisa mwingiliano unasumbua na unaingilia hata masuala ya kiuchumi na kiusalama. Serikali inajua hilo na inachukua juhudi mahususi kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto hiyo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali la kwanza; kumekuwepo na uingizaji wa nguo hasa vitenge na kanga kwa njia za magendo kutoka nje ambavyo vinapelekea ukwepaji wa kodi na hivyo kupoteza mapato, lakini pia vinasababisha viwanda vyetu nchini kutokuwa shindani. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba inatokomeza biashara hii ya magendo ili kuweza kusababisha viwanda vyetu viweze kuzalisha kwa tija? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nchi yetu imekuwa na viwanda maarufu sana Afrika Mashariki na Kati, kama vile Kilitex, Urafiki, Mutex, Mwatex, lakini viwanda hivi vimeshindwa kufanya kazi kwa changamoto mbalimbali ikiwepo mitaji. Ningependa kujua Serikali ina mkakati gani angalau kuweza kutoa dhamana za mikopo kwa viwanda hivi ili viweze kujiendesha kwa tija pia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli sekta ya nguo na mavazi nchini imekuwa na changamoto kubwa ikiwemo hiyo ya kuingiza bidhaa hizo kwa njia ya magendo. Tunajua na tulishaanza kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kudhibiti mipaka au zile sehemu ambazo wanaingiza kiholela katika maeneo ya bandari bubu, lakini pia na mipaka ya kutoka nchi za jirani. Pia kwa sasa kumekuwa na tabia ya kuingiza, kupitisha nguo hizo kwenda nchi za jirani halafu kurudisha nchini. Kwa hiyo tumeshaanza kuchukua hatua ikiwemo kudhibiti kwenye sehemu zote zinazoingiza bidhaa, lakini kuongeza watumishi kwenye Taasisi zetu ikiwemo TBS, FCC na wengine, kuhakikisha tunaongeza udhibiti katika mianya ambayo wanaingiza bidhaa hizo bandia hasa bidhaa za nguo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu viwanda ambavyo havifanyi kazi, ni kweli kuna viwanda ambavyo vimesimama ikiwemo kama alivyotaja ya Urafiki, lakini anajua Serikali tumekuwa na mkakati mara nyingi kuhakikisha tunavisaidia kwa kuweka dhamana na kuweza kuweka ruzuku mbalimbali ili viweze kufanya kazi. Ndiyo maana hivi viwanda tisa ambavyo vinaendelea kufanya kazi sasa, ni kutokana na juhudi hizi za Serikali mpaka vimefikia idadi hiyo kutoka vitatu mpaka tisa, nakushukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mwaka 2014 tuliweza kubadilisha Sheria ya Skill Development Levy ambapo zilikuwa asilimia nne zote ziende VETA kwa ajili ya kuboresha ujuzi na miundombinu ya VETA, lakini 2014 tulibadilisha kwa sababu by then tulikuwa hatuna VETA nyingi na sasa hivi Serikali imejenga VETA nyingi sana.

Je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka warudishe ile sheria tuibadilishe, hizi asilimia mbili ambazo zilipelekwa Bodi ya Mikopo kwa ajili kukopesha wanafunzi wa elimu ya juu ziweze kurudishwa VETA; zitumike kama ilivyokuwa imedhamiriwa awali?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa swali lake la msingi na kuona umuhimu wa taaluma hii ya VETA katika nchi yetu. Hata hivyo, kwanza nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Esther kwanza Serikali imekuwa ikipeleka ruzuku kwenye vyuo hivi, ruzuku zile za uendeshaji, ndiyo kwa maana unaona hata zile ada zake ziko chini sana kwa wanafunzi wa kutwa ni Sh.60,000 na kwa wale wa mabweni ni Sh.120,000. Kwa vile Mheshimiwa amezungumza habari ya sheria kwamba tuirejeshe hapa Bungeni ili tuweze kuirekebisha ili basi ile asilimia nne iweze kwenda kuongeza nguvu kwenye eneo lile la VETA.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tubebe ushauri wake Mheshimiwa Matiko twende tukaufanyie kazi, tufanye tathmini ya kina, tukiona kuna haja ya kuleta hiyo sheria hapa ili tuweze kubadilisha, tuweze kufanya hivyo. Nakushukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; migogoro ya ardhi kati ya Hifadhi ya Serengeti Wilaya ya Serengeti na Wilaya ya Tarime, Bunda umekuwa ni wa muda mrefu na ambao mingine inapelekea hata kuzuia wananchi kufanya shughuli zao, mathalani Kata ya Nyatwali iliyopo Wilaya ya Bunda ambayo ina vijiji vitatu, cha Serengeti, Tamahu na Nyatwali yenyewe ina wakazi takribani 10,000 na Serikali imepeleka miradi ya umwagiliaji takribani wa bilioni 1.7 na maji safi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakazi hao wamezuiliwa kuendeleza makazi yao takribani miaka 10; tunataka kujua ni kwa nini Serikali isiwaache hao wananchi waendeleze na makazi kwa sababu mmeshindwa kuwalipa fidia ili iweze kuondoka takribani miaka 10 sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna maeneo mengo likiwemo eneo la Nyatwali ambalo kiuhalisia lilikuwa ni eneo la wananchi, na nipende tu kuwaambia wananchi wa Nyatwali kwamba hakuna mgogoro isipokuwa wananchi walioko pale wako kihalali kabisa, wanaishi kihalali na Serikali ilishasajili vijiji na wananchi wapo miaka ya tangu 1974, wapo pale. Hilo niwaondoe wasiwasi, hakuna mgogoro isipokuwa yale maeneo hata wewe ni shahidi umekuwa ukiona malalamiko mengi ya Waheshimiwa Wabunge wananchi wao wanalalamika kwamba kwa asilimia kubwa wanachangamoto ya wanyama wakali hususani tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili wananchi wa Nyatwali ni mojawapo ya maeneo ambayo yana kilio hiki, tathmini ya Serikali ni kuangalia namna iliyobora ya kuepusha hawa wananchi wasiendelee kuteseka na wanyama wakali. Maeneo ni mengi yamezibwa yamewekwa makazi ya kudumu, wananchi wamejenga kwenye maeneo ambayo ni mapito ya wanyama ukiangalia eneo la Nyatwali ni eneo moja wapo ambalo upande mmoja ni Serengeti National Park, upande mwingine ndio Nyatwali ilipo na vijiji vya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiruhusu pale wananchi kuendelea kuishi changamoto ya wanyama wakali tutaendelea kulia kila siku kwa hiyo mimi niwaombe wananchi, maeneo yote ambayo tumeyainisha Serikali imesitisha kuleta huduma mbalimbali, Serikali imeshaanza kufanya tathmini wananchi watalipwa kupisha maeneo hayo. Na hili ni tamko la Serikali kwamba ili kupunguza athari za wanyama wakali ni vyema tukatafuta eneo maalum ya mapito ya wanyama kuliachia ili wananchi waishi kwa amani na wanyama waendelee kupita katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tunalishughulikia kwa uhakika na kwa haraka zaidi ili wananchi waweze kuishi kwa amani na Serikali iendelee na taratibu za uhifadhi ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; Mkoa wa Mara ulikuwa na viwanda vinne vya kuchakata Samaki, lakini vyote vimekufa kimebaki kimoja tu cha Musoma Fishing Process kwa sababu ya changamoto mbalimbali ikiwepo ukosefu wa miundombinu rafiki wa uwanja wa ndege ambao ungeweza kusafirisha mazao ya samaki kwenda nje na sasa tunasafirisha malighafi kwenda Nairobi ili yaweze kuchakatwa yatoke nje.

Sasa ningetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba inatatua changamoto mbalimbali ili viwanda vyetu vile vifufuliwe na kuweza kuuza mazao ya samaki na sio malighafi ya samaki? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ni kweli kwamba viwanda vilikuwepo kwenye Mji wa Musoma na ukanda wote wa Ziwa Tanganyika upande wa Mkoa wa Mara na sasa kiwanda kimoja kinaendelea kufanyakazi. Lakini nitoe tu ufafanuzi kwamba viwanda vingi pia havifanyikazi kwa sababu ya matatizo ya kiuendeshaji, matatizo ya kimenejimenti ya wenye viwanda wenyewe. Sababu sio moja tu kwamba miundombinu inayohusiana na kuongeza masoko na kadhalika ndio inayosababisha hiyo. Viwanda vingi vya wawekezaji hasa vya samaki vimekumbwa na tatizo la uendeshaji wa viwanda hivyo, matatizo ya kimenejimenti. Kwa hiyo, Serikali kama Serikali tuko tunazungumza nao na kuona ni kwa namna gani viwanda vile vinaweza vikafufuliwa au basi kuvikabidhi kwa wawekezaji wengine binafsi ili viweze kuendelea kufanyakazi. Kwa sababu…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Kituo cha Polisi cha Kigonga kinahudumia wananchi waliopo mpakani mwa Tanzania na Kenya wa kata za Itirio, Nyanungu, Mlimba na Gorong’a, lakini kituo hiki kilijengwa kwa full-suit ya mabati kana kwamba kimechakaa na polisi wamekimbia hawapo tena pale.

Sasa ningetaka kujua ni lini Serikali itajenga kituo hiki kwa sababu ni kituo cha kimkakati ukizingatia kipo mpakani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, viwango vyetu vya kujenga vituo vya polisi siyo kuwa full-suit ya mabati, kwa hiyo kama kuna kituo cha aina hiyo hakikidhi viwango pengine sasa niwasiliane na Mheshimiwa Mbunge na mamlaka ya Serikali za Mitaa kule Temeke ili tuanze mkakati wa kujenga kituo kwa kutumia vifaa vya kudumu ikiwa ni matofali na kadhalika...

MBUNGE FULANI: Tarime.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Tarime vijijini yes, kwa hiyo nachukua ahadi...

SPIKA: Waheshimiwa hapa mnapenda kuwazungumzisha Mawaziri wakiwa wanazungumza mwache amalize jibu lake, ukiwa unaongea naye anaanza kuongea na wewe badala ya kuongea na mimi hapa mbele.

Mheshimiwa Naibu Waziri malizia majibu yako.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nashukuru nilikuwa nasema hatuna vituo vinavyopaswa kuwa vya polisi vyenye kujengwa kwa full-suit za mabati kwa hiyo kituo hiki kama kweli kipo kule mpakani tutashirikiana na uongozi wa Polisi Kanda Maalum ya Tarime Rorya ili kuwa na mpango wa kujenga kituo hiki kwa aina ya vifaa vinavyostahiki kujengea kituo cha polisi. Kwa hiyo, nimuondoe mashaka Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaweka kipaumbele na kwa vile kituo kiko mpakani, kilete taswira nzuri ya kituo stahiki katika nchi yetu, nashukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya kutoka Tarime Mjini mpaka Mugumu ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Tanzania na Mkoa wa Mara kwa ujumla kwa sababu inaunganisha kwenda kwenye utalii na ilitengewa fedha kuanzia mwaka 2021/2022, takribani bilioni 35, lakini Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa kusuasua mpaka sasa hivi imepeleka bilioni tano tu.

Je, ni lini, Serikali itahakikisha kwamba inampelekea mkandarasi fedha kwa wakati ili aweze kukamilisha ile barabara kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu na hii barabara imegawanywa katika lot mbili, hatupeleki hela yote, tunalipa kulingana na mahitaji ya mkandarasi. Kwa hiyo akishaleta hati ya malipo ndipo tunapomlipa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali itaendelea kulipa kadri hati zinavyokuja kuhakikisha kwamba barabara yote ya Tarime - Mugumu inakamilika, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Tarime inajumuisha Halmashauri ya Mji wa Tarime, Mji wa Sirari, Nyamwaga na Nyamongo, miji ambayo inakua kwa kasi kubwa sana na kusababisha ujenzi wa makazi au hoteli za ghorofa, lakini tumekuwa hatuna gari la zimamoto, na mara kadhaa tunapopata majanga ya moto inasababisha maafa makubwa bila msaada wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua sasa, katika haya magari matano ambayo Waziri amesema hapa, ni lini Tarime itapata, maana mara kadhaa nimesimama nikiomba gari la zimamoto kwenda Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza kwenye jibu la msingi la nyongeza kwamba Serikali ina mpango wa kutumia zaidi ya shilingi bilioni 200 kununua magari na vitendea kazi vingine kuwezesha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Kwa hiyo, fedha hizo zitakapopatikana, Wilaya ya Tarime ni moja ya Wilaya zitakazonufaika, na ninaamini zitapatikana kabla ya mwaka huu wa fedha haujakamilika, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; kutokana na upungufu wa walimu kuna walimu ambao wameendelea kujitolea katika shule za msingi na shule za sekondari kwa kulipwa na wananchi. Sasa ni kwa nini Serikali walau isiwape mkataba wa muda ili kuwapa motisha waendelee kufundisha wakati wakisubiri kuajiri walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, Serikali ilikwishatoa kwanza maelekezo kwa Wakuu wa Shule lakini kwa maana ya Wakurugenzi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwamba wanaweza wakaajiri walimu wa kujitolea kwa muda wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuwaingiza kwenye utaratibu wa ajira za kudumu; kwa hiyo, jambo hilo linaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna ya kuweka mikataba, Serikali imeandaa mwongozo mahususi ambao utapelekea kuandaa mfumo ambao utawezesha walimu wanaojitolea kutambuliwa rasmi kwenye mfumo kuepuka udanganyifu wa baadhi ya Wakuu wa Shule wasiowaaminifu ambao mara nyingi wamekuwa wanaleta majina kwa mfano wakati wa ajira walimu ambao wanajitolea lakini wanaleta pia walimu ambao hawajitolei. Kwa hiyo, tunataka tuwe na mfumo mahususi ambao walimu wenyewe watajisajili na Ofisi ya Rais, TAMISEMI itakwenda kuhakiki na kujiridhisha ili ajira zinapotokea waweze kupata kipaumbele cha kuajiriwa katika ajira za kudumu, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza niseme tu nasikitika na majibu kwa sababu nilielekeza swali langu TANROADS kwa maana ya highways, lakini hapo anajibu vikundi vilivyosajiliwa na Halmashauri, Manispaa na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutumia teknolojia ya kisasa kwa maana ya magari yangeweza kuwa yanasafisha hizi highway usiku ambapo kuna msongamono mdogo sana wa magari. Nataka kujua, Serikali imeshafanya cost benefit analysis kuweza kujua matumizi ya vifaa vya kisasa vis a vis wanavyosafisha kwa mikono ina faida gani kwenye uchumi wa Kitaifa? Kwa maana vifaa vya kisasa vinapunguza msongamano wa magari, ajali na madhara mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali imeshafanya tafiti kuweza kujua madhara wanayopata wananchi wanaofanya usafi kwa mikono kusafisha barabara na mitaro? Wameshafanya tafiti za kiafya kujua madhara wanayopata wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, wazo la Mheshimiwa Mbunge Serikali imelichukua, hilo la kwanza.

Suala la pili, ni kwamba TANROADS pia ina barabara ambazo ziko katika Majiji, Miji, Manispaa na hata katika Halmashauri za Wilaya. Hayo maeneo ndiyo hasa ambayo yameonekana yanakuwa na uchafu mwingi ambayo yanahitaji kufanyiwa usafi. Hata hivyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi ya kufanya usafi wa barabara huwa tunatoa kwa wakandarasi na hawajalazimishwa kwamba ni lazima watumie watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kwa sasa pale Dar es Salaam tayari tuna wakandarasi wawili ambao wameshaanza kutumia teknolojia hii ya kutumia magari kusafisha barabara zetu. Pia, namkumbusha Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna Sheria inayotutaka katika kila mwaka vikundi vingapi, watu wangapi ambao wamepewa kazi hizi za kufanya usafi, kwa hiyo ni takwa pia la kisheria ambalo ni lazima tulitimize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema tutakapokuwa tumejiridhisha, kwamba kuna haja sasa pengine ya kubadilisha sheria kwamba tuelekeze zaidi kwenye matumizi ya vifaa vya kisasa, hilo litafanyika na ndiyo maana tumesema wazo hilo tumelichukua. Hili ni pamoja na kuangalia kama kuna madhara kiasi gani ambayo wanaofanya usafi kwa njia ya mikono ambavyo ni vikundi vya watu maalum hasa vikundi vya akinamama na vijana ambavyo mara nyingi ndiyo vitakuwa vinafanya kazi. Tutafanya hizo tafiti kwa kuwa hilo wazo tumelichukua na tutalifanyia kazi, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Soko la Kimataifa ya Mazao la Lemagu ambalo lipo mpaka wa Sirali ni soko la kimkakati katika kukuza uchumi wa Taifa letu. Soko hilo lilijengwa na kutelekezwa zaidi ya miaka 12 iliyopita; na katika kufuatilia Serikali iliahidi kulifufua. Nataka kujua mchakato umefikia hatua gani katika kufufua soko lile?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, bahati nzuri hili soko mimi nalifahamu. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba alishapatikana mkandarasi anaitwa Nice Construction. Soko hilo litagharimu karibu bilioni 1.04 kwa ajili ya kulijenga na kulimaliza. Kwa hiyo hatua ipo vizuri na kazi itaendelea muda mfupi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Tarime inajumuisha Halmashauri ya Mji wa Tarime, Mji wa Sirari, Nyamwaga na Nyamongo, miji ambayo inakua kwa kasi kubwa sana na kusababisha ujenzi wa makazi au hoteli za ghorofa, lakini tumekuwa hatuna gari la zimamoto, na mara kadhaa tunapopata majanga ya moto inasababisha maafa makubwa bila msaada wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua sasa, katika haya magari matano ambayo Waziri amesema hapa, ni lini Tarime itapata, maana mara kadhaa nimesimama nikiomba gari la zimamoto kwenda Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza kwenye jibu la msingi la nyongeza kwamba Serikali ina mpango wa kutumia zaidi ya shilingi bilioni 200 kununua magari na vitendea kazi vingine kuwezesha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Kwa hiyo, fedha hizo zitakapopatikana, Wilaya ya Tarime ni moja ya Wilaya zitakazonufaika, na ninaamini zitapatikana kabla ya mwaka huu wa fedha haujakamilika, nashukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule za msingi ambazo ni kongwe zimejengwa miaka ya 1960 na 1970 ambazo hazifai kabisa kukarabatiwa bali inabidi Serikali iende na mkakati wa kuzijenga upya. Mathalan Shule ya Msingi Nyabilongo, Kikomori na Kiongera zilizopo Kata ya Susuni, Jimbo la Tarime Vijijini. Ni shule ambazo ni hatarishi hata kwa wanafunzi wanaposoma katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba inapeleka fedha kwa uharaka ili hizi shule kongwe ziweze kujengwa na kuweza kunusuru maisha ya wanafunzi wale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko, kwanza niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika kipindi hiki cha uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ndiyo kipindi ambacho Serikali hii ya Awamu ya Sita imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 230 katika ujenzi wa shule mpya na ukarabati wa madarasa kwenye Elimu Msingi kuliko wakati mwingine wowote ule. Hivyo basi, nimtoe mashaka Mheshimiwa Matiko, shule hizi alizozitaja tutaziweka katika mpango na kuona ni namna gani fedha inazifikia kwa ajili ya ukarabati wa madarasa na ujenzi wa majengo mapya katika shule hizi. (Makofi)