Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Esther Nicholus Matiko (6 total)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa na mimi nimwulize Waziri Mkuu swali.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni dhahiri kwamba wanafunzi hawatakiwi kufanya siasa Vyuoni, lakini kumekuwepo na ama mkakati au maelekezo ambapo Menejimenti ya Vyuo inawanyanyasa wanafunzi wanaokuwa hawapendezwi na siasa ya Chama cha Mapinduzi. Je, ni kweli kwamba kuna hayo maelekezo? Kama hakuna maelekezo, Serikali inazieleza nini sasa Menejimenti za Vyuo kuhusu hii tabia ambayo imejengeka ya kuwanyanyasa vijana na hata kuthubutu kuingilia Uongozi wa Serikali za Wanafunzi? Mojawapo ya Chuo ambacho kimekithiri ni Chuo Kikuu cha Dodoma.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Tarime, kama ifuatavyo:-
Kwanza nataka nikanushe kwamba siyo kweli kwamba kuna maelekezo kwenye Vyuo vyote vya Elimu ya Juu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, hakuna unyanyasaji wowote unaofanywa kwenye Vyuo kwa wanafunzi ambao...
Mheshimiwa Spika, narudia tena. Hakuna unyanyasaji wowote wa Vyuo...
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, Watanzania wote wanao uhuru wa kujiunga na vyama vyovyote wanavyovitaka, lakini kila eneo limeweka utaratibu wake. Hakuna zuio la wafanyakazi kujiunga na vyama vyovyote lakini liko zuio la mtumishi anapokuwa kazini kuendesha siasa. Hakuna zuio la mwanafunzi yeyote kama Mtanzania kujiunga na Chama anachokitaka yeye, lakini zuio ni kwamba hutakiwi kufanya siasa wakati wa masomo ili u-concentrate na masomo yako. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, inaweza kutokea labda vijana wawili wenye itikadi tofauti huko wakafanya mambo yao, wakatofautiana huko, huo siyo utaratibu wa Serikali, ni utaratibu wao wao wenyewe. Kwa hiyo, nawaomba sana niwasihi Viongozi wa Vyama vya Siasa, tusilione hili kama ni msimamo wa Serikali, badala yake tulione hili kama ni mapenzi ya watu wengine, kama ambavyo vijana wafanyabiashara huko wanavyoweza kukorofishana mahali pao, lakini haina maana kwamba yule wa Chama Tawala anapokorofishana na mtu mwingine wa Chama cha Upinzani huko kwenye biashara zao tukasema labda soko lile, Chama Tawala kimepeleka watu wake kuzuia watu wa Vyama vingine wafanye vurugu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwisho, niwasihi Watanzania wote; Tanzania hii ni yetu sote na tunahitaji maendeleo ya Watanzania wote. Kila mmoja anao uhuru wa kupenda Chama anachokitaka. Kama kuna maeneo yanabana kisheria na kwa utaratibu wa matumizi au matakwa hayo kuyapeleka maeneo hayo, lazima yazingatiwe. Serikali hii itaendelea kuwatumikia Watanzania wote bila kujali Vyama vyao; tutaendelea kuwahudumia Watanzania wote bila kujali Vyama vyao; pia tutatoa elimu kutoka ngazi ya awali mpaka elimu ya juu bila kujali mapenzi ya Chama chako. (Makofi)
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikusihi tu uamini bado kwamba Serikali hii haina jambo hilo wala haina maagizo hayo mahali pa kazi na uwe na amani. Nami nasema Watanzania hawa ni ndugu, wanaishi pamoja na bado tunapenda washiriki kikamilifu katika masomo yao. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni wajibu wa Serikali kuyahudumia majeshi yetu kwa kuyapatia uniform ambazo ni viatu, soksi, suruali au sketi, shati, mkanda wa suruali, mkanda wa filimbi, nembo ya cheo, lakini na kofia. Imekuwa ni muda mrefu sasa majeshi haya hayapatiwi hizi uniform badala yake wanajinunulia wao wenyewe.

Mheshimiwa Spika, mathalani Jeshi la Magereza tangu 2012 hawajawahi kupatiwa uniform, vivyohivyo kwa Jeshi la Polisi na hizi uniform wanajinunulia kwa bei ghali sana. Mathalani nguo ambazo za jungle green wananunua kwa 70,000/=, kofia 15,000/=, buti zile 70,000/= na hawa askari wetu wanafanya kazi kwa mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Spika, ningetaka kujua sasa ukizingatia Askari Magereza kwa mfano mwenye degree analipwa sawa na Askari Magereza mwenye elimu ya kidato cha nne, shilingi 400,000 aweze kununua, ajigharamie nyumba na mambo mengine.

Ni nini sasa Kauli yako Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhakikisha kwamba, askari hawa wanapewa uniform zao, maana ni stahiki ambayo wanatakiwa kupewa, sanjari na kurudishiwa gharama zote ambazo wamekuwa wakijinunulia hizi uniform kwa kipindi chote ambacho Serikali ilishindwa kuwapa hizi uniform?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Tarime, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kimsingi Serikali inao wajibu wa kutoa vifaa mbalimbali ikiwemo sare kwa majeshi yetu, ili waweze kufanya kazi yao kwa urahisi zaidi. Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo inasimamia Jeshi la Polisi, Magereza pamoja na Uhamiaji pamoja na Zimamoto ni Wizara ambayo inaendelea kuratibu namna nzuri ya kupata sare na vifaa mbalimbali, ili kuwawezesha watumishi wetu askari kwenye majeshi hayo waweze kufanya kazi yao. Na sera yetu ni kwamba, bado Serikali itaendelea kuwagharamia.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ni shahidi mwaka jana tumekuwa tukijadili upande wa Jeshi la Polisi, Wizara ya Mambo ya Ndani ilipokuwa imeagiza, imetoa zabuni ya kununua sare na tukapata taarifa kwamba, kuna majora yako pale ambayo yameandaliwa kwa ajili ya kuwapa askari, hiyo ni dalili kwamba, Wizara ya Mambo ya Ndani bado inatoa huduma hizo kwa askari wake.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna mahali ambako kwa Wizara upande huo wananunua hizo sare tutaweza kuwasilisna pia na Waziri mwenye dhamana, ili tuone kwa utaratibu huo ukoje na kwa nini sasa askari wanunue na kama ndio sera ya ndani ya Wizara tutaweza kujua na tunaweza tukafanya marekebisho kadiri ya mahitaji yalivyo, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua Serikali ina mamlaka ya kutoa ardhi kutoka kwa wananchi kwa ajili ya matumizi mbadala kama vile ya uwekezaji au matumizi mbalimbali kwa taasisi za umma na binafsi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999, Sheria Na.4 Kifungu cha 3(i) na (g) kinatamka bayana kwamba pale mtwaaji anapochukua ardhi kutoka kwa wananchi lazima ahakikishe amefanya uthamini wa haki na ukamilifu, lakini zaidi ahakikishe analipa fidia kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na haya mazoea ya kufanya uthamini lakini inachukua muda mrefu sana kulipa fidia katika maeneo haya ambayo Watanzania wamechukuliwa ardhi zao, ili waweze kwenda sehemu zingine na kuweza kuanzisha makazi na kufanya shughuli za kijamii na uchumi:-

Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujua, ni nini hatua ya Serikali kuhakikisha kwamba pale tathmini inapofanyika basi hawa wananchi wanalipwa fidia zao kwa wakati ili waweze kwenda kuendelea na shughuli za kiuchumi? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunayo Sheria ya Ardhi na imetoa maelekezo kwa watumiaji wote. Kwa sera ya Serikali yetu nchini, ardhi ni mali ya Serikali na ni tofauti sana na maeneo mengine na kila mtumiaji wa ardhi hii ni lazima apate kibali, sisi tunaita hati, ile hati ni kibali cha matumizi ya ardhi ambacho kinaeleza umepewa ardhi hiyo kwa ajili ya nini? Mfano, kujenga nyumba; kiwanda au shamba, kile ni kibali cha Serikali kwa mtumiaji. Huo ndiyo utaratibu ambao tunao na ndiyo maana tunasisitiza kila aliyejenga nyumba, mwenye shamba, anataka kufanya biashara ya kiwanda, lazima apate hati, yaani apate kibali kutoka Serikalini.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ardhi hii ni ya Serikali, inaweza kuwa na mahitaji ya uendelezaji kwenye eneo ambalo tayari watu wapo, wanafanya kazi zao za kilimo yaani wanaendelea na maisha yao ya kawaida. Pale ambapo tunahitaji ardhi hiyo na hapo pana watu wanafanya shughuli zao, ili kuwatoa tunafanya uthamini. Katika zoezi la uthamini ni lazima uende kujua eneo hilo la ukubwa huo ambako mwananchi huyo yupo; kama alipanda mazao; mazao yote yamewekwa bei maalum ya uthamini; lakini pia kama amejenga nyumba, inafanyiwa uthamini na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inapotaka kufanya jambo hilo, au yeyote anapotaka kutumia eneo hilo ambalo mwananchi yupo, suala la uthamini limezungumzwa pia na limesisitizwa na hili lazima lizingatiwe kwamba mtu anapotolewa eneo moja kupelekwa eneo lingine kwa lengo la kutumia eneo hilo iwe ni kwa uwekezaji au kufanya kazi nyingine, ni lazima uthamini uwepo. Najua yapo matatizo kadhaa katika maeneo mbalimbali, wengine huchukua ardhi bila fidia, wakati mwingine kunaweza kuwa na makubaliano, wakati mwingine wananchi wenyewe wanaamua kutoa ardhi ili shughuli muhimu ifanywe.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge kama analo eneo ambalo kuna malalamiko na yanahitaji wananchi wa eneo hilo kupata haki yao stahiki, bado una fursa ya kuonana na viongozi wa eneo hilo waanze utaratibu wa kwenda kufanya uthaminishaji ili wananchi wote waweze kulipwa fidia yao kulingana na ukubwa wa ardhi na thamani ya mali zilizopo.

Kwa hiyo, hili limesisitizwa na linasimamiwa maeneo yote ili kila mmoja apate haki yake kulingana na ukubwa wa eneo lililoachwa kwa ajili ya shughuli hiyo mpya. Huo ndiyo utaratibu tulionao ndani ya Serikali. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kumekuwepo na uhaba wa rasilimali watu kwenye taasisi za idara mbalimbali za Serikali, mathalani kada ya walimu, watumishi wa afya na kwenye majeshi yetu; Jeshi la Polisi, Magereza na JWTZ kitu ambacho kinapunguza ufanisi katika kutoa huduma kwa wananchi. Hata jana Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani alikiri kabisa kwamba kuna upungufu ambao unapelekea hata kufunga vituo vya polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imechukua hatua kwa kutangaza ajira 3,000 kwenye Jeshi la Polisi lakini kuna masharti ambayo yameambatana, kwanza wamesema ni ambao wamemaliza JKT na JKU lakini sharti namba tano na sita linaeleza kwamba ni wale vijana waliomaliza form four na form six kati ya mwaka 2017 na 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunatambua kwamba ajira zilisitishwa tangu mwaka 2015 na kuna vijana ambao wamemaliza form four na form six kati yam waka 2015/2016 na wameenda JKT na JKU na zaidi wamejenga Taifa letu kwa mfano Oparesheni Magufuli, Operesheni Makao Makuu na Operasheni Mererani.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwa nini sasa Serikali isifanye rejea kwenye tangazo lao la ajira ambalo lina-limit vijana hawa wa 2015/2016 ili liweze kuwa-accommodate na wao? Kwa nini wasiseme kwamba ajira inatolewa kwa vijana wote wenye sifa kuanzia waliomaliza form four na six 2015 mpaka 2020? Mfano Iringa na Mbeya wamewakataa walivyoenda kwenye usaili. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali inaendelea na zoezi la kuajiri watumishi wa sekta mbalimbali hapa nchini ikiwemo na hayo matangazo aliyoyasema ya Jeshi la Polisi. Sina uhakika na vigezo hivyo na wito walioutoa kwamba wanataka waajiri vijana kuanzia mwaka gani lakini tuichukue hiyo kama ushauri kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo sasa inasimamia ajira hiyo ili waanze kufanya mapitio ya ajira hiyo na vigezo ili pia hawa waliomaliza jeshi kuanzia mwaka 2015 nao waingie halafu wachujwe wote tupate vigezo na tuweze kuwapata wale ambao wana sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua pia tulikuwa na hilo kundi la Operesheni Magufuli na Operesheni Mererani na wote waliahidiwa kuingia kwenye orodha ya ajira na kama miongoni mwa hao walianza mwaka 2015 na kumaliza 2016 na hao walioanza kuchukuliwa 2017 mpaka sasa basi Wizara naona itatimiza wajibu wake kuwaita wote halafu iwachuje waweze kupata ajira pia. Kwa hiyo, tunaupokea ushauri wako na Waziri wa Mambo ya Ndani yuko hapa atalichukua hilo kwa ajili ya kulifanyia kazi. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2014 tulitunga Sheria ya Tozo ya Ujuzi na Maendeleo ambapo mwajiri wa sekta binafsi wenye wafanyakazi zaidi ya kumi walitakiwa kuchangia asilimia nne kwa mujibu wa kifungu cha 14 cha VETA. Lakini asilimia mbili zilielekezwa kwenda kwenye Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.

Kwa kuwa sasa Serikali imejenga VETA nyingi nchini; na kwa kuwa ofisi yako sasa hivi imetoa fursa kwa vijana wengi kuweza kujiunga na mafunzo haya ya muda mfupi ili waweze kujiajiri na kuajiriwa.

Ni kwa nini sasa Serikali isione ni muda muafaka wa kurejesha ile asilimia mbili ile iliyopelekwa kwenye bodi ya mikopo iweze kurudi VETA ili waweze kutumia kukopesha wanafunzi hawa vifaa ambavyo watajifunzia na baadaye waweze kuondoka navyo kwenda navyo mtaani vya kuanzia kazi? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulitunga sheria inayotengeneza mgao wa fedha ambazo pia tungependa tuzione zikitumika kwenye vyuo vyetu vya elimu hasa kwenye ufundi stadi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa Serikali utakaowezesha vijana wanaohitimu VETA baada ya kuwa tumejenga VETA nyingi nchini namna ya kuwasaidia wanaohitimu ili waweze kuanza vizuri.

Mheshimiwa Spika, kimsingi Serikali imeanza kuimarisha sekta hii ya ujuzi kwa utaratibu, mwanzo tumeanza kujenga VETA na tulianza kujenga VETA kila mkoa, kazi ambayo tumekamilisha siku chache zilizopita; na mimi nimepata nafasi ya kupita mikoa mingi kuona maendeleo ya ujenzi; lakini pili tumeanza na programu ya ujenzi wa VETA kila wilaya zoezi ambalo sasa linaendelea. (Makofi)

Msimu uliopita tulipata fedha, Waheshimiwa Wabunge mlipitisha bajeti ya kujenga VETA 28 kazi ambayo inaenda mwishoni ili pia tuweze kujenga VETA nyingine.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme tunaenda kwa awamu, tumeanza na ujenzi wa miundombinu, lakini mbili tunatoa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, halafu tuje tuone sasa tuna idadi gani ya wanafunzi wanaohitimu, tuweze kutenga fecha pamoja na hiyo tozo ambayo pia tunatoza na ile asilimia tunayoitenga tuiingize kwenye mpango huo ili kutoa vifaa vitakavyowezesha kijana huyu anayehitimu kuanza mafunzo yake na stadi yake mara tu anapohitimu. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kulifanyia kazi jambo hili ili kuona hawa vijana wetu wanaoingia kwenye vyuo hivi kwa ajili ya kupata ufundi stadi anapomaliza anaanza kazi moja kwa moja.

Kwa hiyo kadri tunavyoendelea Wizara ya Elimu ambayo ndiyo inashughulikia elimu ya ufundi kupitia VETA itaendelea kuratibu na kuomba fedha zaidi na tunashukuru mmetupitishia bajeti ya Wizara ya Elimu katika sekta mbalimbali ikiwemo kwenye eneo la ujuzi, ili tuweze kuhakikisha kwamba vijana wa Kitanzania wanakuwa na ujuzi katika fani mbalimbali ambazo wao wanazihitaji ziwasaidie pia kwenye kujitafutia ajira au pia wao wenyewe kuwaajiri wengine, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Tunatambua kwamba vijana ambao wanakuwa wamemaliza kidato cha sita na wengine wanawajibika kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa ili kuweza kujifunza uzalendo, umoja wa kitaifa, stadi za kazi, stadi za maisha lakini cha zaidi utayari wa kulitumikia Taifa.

Mheshimiwa Spika, tarehe 31 Juni kuna wito umetolewa na JKT kuwaita vijana waliomaliza kidato cha sita kujiunga na JKT, lakini umeambatana na orodha ya mahitaji mengi sana ambayo wanatakiwa waende nayo. Tunatambua kwamba ni muhimu sana vijana hawa kujiunga na JKT na hapo zamani ilikuwa ikitolewa na vijana wanaenda kuripoti kambini vifaa vyote vinatolewa kule kambini.

Sasa nilitaka tu kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni kwa nini sasa Serikali isione kwamba ni muhimu kuwajengea uwezo hawa vijana ili tuweze kuwaacha wale vijana ambao wanatoka kwenye kaya maskini iweze kutoa vifaa hivi kama ilivyokuwa ikitoa hapo zamani? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa wito kwa vijana wetu kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kwa malengo ambayo Mbunge ameeleza kujenga uzalendo, kumjengea uwezo wa kujiamini ili pia kushiriki katika ulinzi wa Taifa lake na tunapofanya hili tunawapeleka kwenye makambi yetu.

Mheshimiwa Spika, Mbunge akitaka kujua kwa nini sasa tunapowaita tunaambatisha na orodha ndefu ya vifaa vinavyotakiwa jeshini. Serikali tumejipanga na tumeandaa utaratibu wa kuwahudumia hawa na vifaa vilivyo muhimu vya shughuli ile ya kijeshi kama bukta, viatu pamoja na sare yenyewe zile ambazo zinatumika kwenye shughuli yenyewe ya mazoezi na uimara na ukakamavu.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali tumetoa nafasi ya watu kuja na vifaa ambavyo tunaweza kuvitumia viko vifaa ambavyo tumewaambia kwamba ukija kwenye eneo hili unatakiwa kuja na moja, mbili, tatu, nne ili uweze kuishi kwenye maeneo haya. Lakini vile vifaa muhimu vyote vinapatikana kwenye eneo lile la ulinzi.

Kwa hiyo, tofauti ya vifaa vile vinavyoagizwa na vile ambavyo vipo ni kwamba vilivyopo ni muhimu kwa mazoezi lakini kuna vile ambavyo vina-support wakati wote kijana huyu akiwa jeshini navyo pia anaweza kujitafutia ndio tunaorodheshea kwamba wanapokuja Makutupora uje na hiki na hiki kulingana na mazingira hayo.

Mheshimiwa Spika, hata sisi tulipokuwa jeshi wakati ule tuliagizwa na tulienda navyo na tulipata vifaa vingine jeshini. Kwa hiyo, ni utaratibu wa kawaida kuagiza vifaa muhimu vya jeshi ambavyo vinapatikana pale pale jeshini, lakini vile ambavyo ni muhimu kwa kuishi kwenye eneo lile basi tunakuagiza uweze kuja navyo ili uweze kuvitumia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kutoa majibu hayo. (Makofi)