Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Vedastus Mathayo Manyinyi (35 total)

MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Pale Musoma Mjini tumekuwa na tatizo la maji kwa muda mrefu na bahati nzuri tumepata mradi ambao tulitegemea toka mwaka jana ungekuwa umekamilika na watu wameanza kupata maji. Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba mradi huo umekamilika kama ilivyokuwa ahadi yake ya toka mwaka jana?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeanza kupata fedha, kwa hiyo, wakati wowote ule tutatuma fedha na kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha tutakuwa tumekamilisha mradi huo.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, namshukuru Naibu Waziri na mimi nakubaliana naye alivyosema kwamba barabara ile ina umuhimu mkubwa hasa ukilinganisha kwamba kuna uzalishaji wa samaki katika eneo hilo, lakini vilevile ni eneo ambalo linapita nchi yetu ya jirani.
Sasa ukiangalia toka 2009 hadi leo, zaidi ya miaka mitano ni kilometa 7.5 peke yake ndiyo barabara iliyowekewa lami, napenda kufahamu Serikali itakuwa tayari kwa mwaka huu kutenga fedha kwa ajili ya hicho kipande cha barabara ili kiweze kujengwa zaidi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, naomba ikumbukwe kwamba mbali na ujenzi wa barabara katika maeneo mbalimbali ambayo yako katika mpango lakini kutokana na umuhimu Mheshimiwa Rais mwaka jana tuliweza kumpa maombi maalum hasa kwa pale Musoma Mjini, tulimpa ombi la barabara ya kutoka Bweri - Makoko ambapo kipande kile zipo sekondari zisizopungua 14, je, Serikali sasa itakuwa tayari kutimiza ahadi hiyo kuanzia mwaka huu wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yake yote mawili yanaongelea kutenga fedha kwa mwaka huu wa 2016/2017 kwa ajili ya kuendelea kujenga ile barabara ya Mika – Utegi – Shirati - Kirongwe pamoja na hii barabara aliyoiongelea ya Bweri - Makoko. Naomba kumuahidi kwamba hivi sasa tunavyoongea, wataalam wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, sekta ya ujenzi, wapo katika hatua ya mwisho ya kuangalia katika haka kasungura kadogo tulikokapata ni wapi tutenge kiasi gani. Kwa hiyo, naomba asubiri Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano itakapokuja itatoa majibu sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pengine moja ningependa kusisitiza, mahitaji ya ujenzi wa barabara ni makumbwa sana sehemu mbalimbali za nchi na priority (kipaumbele) kwa mwaka ujao wa fedha ni kukamilisha miradi ya muda mrefu ili kuondokana na gharama za makandarasi wanazotudai kutokana na kuchelewa kukamilisha miradi. Hivyo, tutahakikisha kwamba barabara zile ambazo zimeanza muda mrefu lazima kwanza zikamilike kabla hatujaingia katika eneo jipya.
MHE.VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, na ameendelea kusema hapa kwamba hii michango tunahitaji kuendelea kuwahamasisha wananchi ili waweze kuchangia. Lakini ukiangalia kwa mapungufu tuliyokuwanayo kwa maana ya madawati, vyumba vya madarasa pamoja na maabara; ni mapungufu makubwa sana na kwa sababu wananchi wengi wanaamini kwamba michango ni hiari kama alivyosema Naibu Waziri, hatuoni kama tutashindwa kutekeleza azma yetu ya kuhakikisha kwamba wanafunzi wote wanaweza kupata elimu bora kwa sababu wanafunzi wengi wataendelea kukosa vyumba vya madarasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tunatambua kwamba wazazi pamoja na shughuli kubwa wanazozifanya pamoja na kujenga hostel, lakini bado ukiangalia wale wanafunzi wa kike zile gharama zote za kuwasomesha kwenye zile hostel bado ni gharama za wazazi. Ni kwa nini Serikali isikubali kugharimia hizo gharama za hostel baada ya kuwa hizi hostel zimejengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Mathayo kwa sababu katika rekodi pale juzi juzi ameweza kushiriki utoaji wa mifuko 200 ya cement kwa ajili ya ujenzi wa madarasa katika eneo lake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefika pale Musoma Mjini, nimeweza kutembelea nimeona kazi kubwa anayofanya. Kwa hiyo, imani yangu kwa ile kazi unayoifanya na nadhani mnataka mjenge takribani vyumba karibuni 200 vinatakiwa vikamilike ndani ya mwezi Machi, naomba tuwaunge mkono kwa sababu mnafanya kazi njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kusema kwa mkakati huu tutashindwa, naomba nikuhakikishie ndio maana mwaka huu tunakamilisha vyumba vingi kwa kutenga karibu shilingi bilioni 29, na ndugu zangu Wabunge naomba niwaambie huku site tunakotoka sasa hivi ukienda huko utakuta kazi kubwa sana ya ujenzi wa madarasa inaendelea. Naamini katika muda huu ambao tuko hapa Bungeni, Mbunge mwingine akirudi katika site kwake atakuta kwamba kuna madarasa mengine katika eneo lake hata alikuwa hajatarajia yameshakamilika. Hii yote ni juhudi ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niwahakikishie Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali tutajitahidi kuhakikisha azma ya Serikali kuwapatia wananchi wake elimu bora inafanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala zima la zile hostel zilizojengwa changamoto ni kubwa sana, katika suala la vijana hasa watoto wetu wa kike kwamba ikiwezekana kwamba zile hostel zilizojengwa Serikali igharamie. Naomba niseme hili ni wazo ngoja tutalifanyia kazi, kwa sababu kugharamia hostel zote Tanzania ni bajeti kubwa sana na hizi zimejengwa makusudi ni hostel za kata ziko katika maeneo yetu. Lengo ni mtoto anaenda shuleni na kurudi lakini kwa sababu changamoto ya uzito kwa wanafunzi ni vyema tujenge hostel nasema tuendelee na mpango huu wa sasa pale Serikali kwa kushirkiana na wadau mbalimbali itakavyoona kwamba nini tufanye, lengo ni kuboresha wananchi katika kata zetu tutafanya hivyo kwa kadri inavyowezekana.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Kule Musoma nako tumekuwa na tatizo kubwa sana la nyumba za askari na kwa bahati nzuri Serikali iilisikia kilio chetu. Hivi ninavyozungumza ni zaidi ya miaka mitatu sasa kuna jengo kubwa la ghorofa ambalo limejengwa pale Musoma Mjini. Cha kushangaza mpaka leo askari wetu hawajakabidhiwa. Nataka kujua Serikali inasubiri nini kukabidhi jengo hilo ili liweze kusaidia kuondoa ile adha kubwa wanayopata maaskari wetu?
Waheshimiwa Wabunge linapofika suala la maslahi ya askari, robo ya tatu ya Bunge huwa wanasimama kutaka askari wetu wapewe maslahi hayo. Nitakapokuwa nakutana nao nitawaambia kwamba Wabunge huwa wanawasemea ili mnapopita majimboni wawape ushirikiano. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu jengo la Mara, kuna hatua za ukamilishwaji ambazo ndiyo zilikuwa zinafanyika kutoka kwa mkandarasi wetu. Ni moja ya majengo ambayo yapo kwenye hatua za ukamilishwaji na yatakapokuwa yamekamilika yatakabidhiwa ili askari wetu wasipate shida hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwa sababu wengi mlikuwa bado mnafuatilia, nimeshazunguka mikoa yote kasoro mikoa minne na kwa Mheshimiwa Sikudhani nitafika, bado Ruvuma, Njombe, Songwe, Geita pamoja na Singida. Nimetambua ukubwa wa tatizo hili na sisi ndani ya Serikali tunaendelea kuwasiliana kuweza kuhakikisha kwamba tunalibeba kwa ukubwa wake na hivyo tutalifanyia kazi ili kuweza kupatikana jawabu la kudumu linalohusu makazi ya askari wetu ili waweze kuendana na hadhi ya kazi wanazozifanya.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kilimo cha mabondeni ni kilimo ambacho ni cha asili na kimezoeleka na wananchi, hasa wa Mikoa ya Iringa, Njombe, Songea na kinajulikana kwa jina la ukulima wa vinyungu, sasa hivi kimezuiwa kutokana na kuzuia uharibifu wa vyanzo vya maji; na kwa kuwa, kilimo hicho ndiyo kimekuwa kikitumika kwa muda mrefu.
Je, Serikali ili kuwanufaisha wananchi wa vijiji vya Lukani, Kihesa Mgagao, Lulanzi, Idete, Kimala, Boma la Ng’ombe, wameweka mikakati gani mbadala kuhakikisha kwamba hawa wananchi wanaendelea kulima kilimo kisasa? Imejipangia mikakati gani? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa lazima tukubaliane kwamba ili tuwe na maji endelevu ya kuweza kuwatosheleza Watanzania ni lazima tutunze vyanzo vya maji. Katika utunzaji wa vyanzo vya maji, kuna watu ambao kwa miaka mingi kama anavyosema wamekuwa wanalima kilimo cha vinyungu; maana yake wanalima kwenye vyanzo vya maji. Sasa mikakati ya kuweza kuwatafutia shughuli mbadala ni lazima muwe shirikishi kati ya Halmashauri na Serikali. Haiwezi kuwa Serikali tu inawapelekea kwamba mtafanya hiki, kwa hiyo, ni lazima iwe shirikishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakwenda kukaa na Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo tuweze kuona shughuli nyingine ambayo wanaweza wakafanya nyingine tofauti na uharibifu wa vyanzo vya maji. Kulingana na sheria yetu, ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji, haturuhusiwi kufanya kazi yoyote, kufuga mifugo au kulima ili tuwe na maji na rasilimali ya kutosha kuwapelekea Watanzania.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba umeme wa REA ni wa vijijini, lakini yako maeneo ya mjini ambayo yana maeneo mengi na makubwa ya vijijini. Nashukuru kwamba REA wameweza kutupatia umeme katika mitaa michache kama ya Nyabisare pamoja na kule Bukanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, kwa kuwa, maeneo mengi ya taasisi yako kwenye hizo kata za pembezoni, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba REA wanaweza kutupatia umeme katika maeneo yote hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa yako maeneo, najua Tarime mko wawili na kuna Musoma na Tarime lakini ki-TANESCO ni Tarime, hakuna shida Mheshimiwa, nimeshakuona Mheshimiwa Esther Matiko.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kusema kwamba, ukweli yako maeneo ambayo yako pembezoni ingawaje yanasemeka yako mjini. Tumeshakaa na Mheshimiwa Manyinyi, yako maeneo na hasa kwa taasisi za umma, taasisi zote za umma zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini viko vijiji ambavyo itabidi tuviangalie, vile vijiji ambavyo vinaonekana viko mjini vitapelekewa umeme kupitia miradi ya TANESCO lakini vile vya vijijini kama ambavyo amesema Nyabisare na vingine, tutachambua ili kuona ni vijiji gani vipelekewe kwa Mradi wa REA. Vijiji vyote vya Miradi ya REA tumeshakabidhiwa, kwa hiyo, kwa Mheshimiwa Mbunge ambaye anaona kuna sehemu kuna utata ni vema tukae ili isionekane kijiji fulani kinarukwa.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Nadhani wote tunatambua umuhimu wa Wenyeviti wa Mitaa na kazi wanazozifanya, lakini kumekuwa na kilio cha muda mrefu sana kuhusiana na maslahi yao kwa kazi kubwa wanayoifanya. Je, Serikali sasa iko tayari kutenga bajeti kwa ajili ya kuwalipa mishahara Wenyeviti wa Mitaa pamoja na Madiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili nililijibu takribani wiki mbili zilizopita na nikasema kwamba kwa jambo la kulipa mishahara utaratibu wa sasa ni kulipa posho. Pale Bunge litakapoamua vinginevyo, tutaangalia jinsi ya kufanya. Kikubwa zaidi ni kwamba tutaendelea na utaratibu huu, lakini tujue kwamba endapo jambo hili litaingia katika mshahara maana yake ni kuwa wage bill lazima itabadilika katika utaratibu wa kiserikali, ambayo vile vile ina changamoto yake. Kwa hiyo lazima tufanye analysis ya kutosha juu ya namna ya kufanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa utaratibu
wa sasa hivi tutaendelea kwa mujibu wa sheria inavyozungumza. Bunge litakapoamua hapo baadaye tutaenda na maamuzi hayo ambayo Bunge litakuwa limeamua hapo baadaye.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Serikali kwa maana ya TAMISEMI wametoa muongozo katika makusanyo yale ya Halmashauri kwa maana ya kwamba asilimia 60 zinapaswa kwenda kwenye maendeleo, asilimia 20 zinapaswa kwenda kwenye kata, asilimia 10 zinapaswa kwenda kwa vijana na wakina mama, kwa hiyo Halmashauri inabakia na asilimia 10 peke yake ambayo ndiyo sasa ilipe mishahara na kuendesha Halmashauri. Je, kutokana na hali hiyo ni kwanini sasa hawa Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wasilipwe moja kwa moja kutoka Serikali Kuu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ukiwaangalia
hao Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wanayo majukumu mengi na makubwa kwa hiyo hata wakati mwingine wanashindwa kutekeleza majukumu yao kutokana na tabu walizonazo hasa hasa za usafiri. Je, Serikali sasa imejiandaaje kuhakikisha kwamba nao inawawezesha kupata usafiri ili waweze kutekeleza majuku yao ya kila siku?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ni kwamba kwanini sasa hawa Wenyeviti wasilipwe moja kwa moja kutoka Serikali Kuu na msingi umesema kwamba kwa sababu kulikuwa na suala zima la mgawanyo wa zile fedha kwamba asilimia 60 ziende katika maendeleo;
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipowasilisha bajeti yetu mwaka Mheshimiwa Waziri alitoa ufafanuzi hapa kwa kina kwamba hili limeonekana kwa sababu lilikuwa hoja ya msingi ya Waheshimiwa Wabunge, ndiyo maana tumetoa maelekezo. Mheshimiwa Waziri alizungumza wazi hapa kwamba fedha hizi sasa zitagawanyika tofauti, kwamba kwa baadhi ya Halmashauri hasa zile ambazo uwezo wake ni mdogo, sasa asilimia 60 zitakwenda katika matumizi haya mengine na asilimia 40 itakwenda katika maendeleo, huu ndio ufafanuzi kulingana na bajeti ya mwaka huu tuliyoipitisha hapa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata hivyo, lengo letu kubwa katika dhana ya ugatuaji wa madaraka ni kutafuta jinsi ya kufanya katika kuongeza nguvu za Halmashauri za kuweza kukusanya mapato. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mathayo tutaendelea kulisimamia hilo, lakini kubwa na la msingi ni jinsi ya kufanya katika kukusanya vizuri mapato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hoja ya pili, kuhusu vyombo vya usafiri; ni kweli, tukiangalia viongozi wetu wana changamoto kubwa ya usafiri, kwa sababu kama Madiwani wanafanya kazi kubwa, lakini hili naomba tulichukue sisi Serikali kwa sababu ni jambo ambalo naona ni la msingi hapo baadaye kwa kupitia Halmashauri zetu ni kwa jinsi gani tutafanya kupitia mifuko mbalimbali ili aangalau kuwezesha Waheshimiwa Madiwani waweze kupata vyombo vya usafiri. Hata hivyo jambo hili tutashirikishana vizuri kupitia katika Serikali zetu za Mitaa.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja la nyongeza. Ni ukweli usiopingika kwamba ufugaji wa samaki ni zao linaloweza kuleta matokeo ya haraka kwanza si katika tu suala la ajira lakini vilevile katika kipato cha mfugaji hata yule mwenye kipato cha chini. Hata hivyo, liko tatizo moja kubwa sana la chakula cha samaki. Taasisi nyingi zikiwemo hizi zetu za Serikali ambazo zinaonesha utafiti wa ufugaji wa samaki wanakuonesha kwamba samaki hasa aina ya tilapia anapaswa afugwe ndani ya miezi sita awe ameshafikia uzito usiopungua nusu kilo kwa kula chakula chenye formula hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza unapokuja kwenye hali halisi wale samaki wanalishwa zaidi mpaka wakati mwingine mwaka mmoja pasipokufikia uzito ule. Kutokana na hali hiyo wakulima au wafugaji wengi wanakata tamaa katika hili zoezi zima la ufugaji wa samaki. Je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuhakikisha utafiti madhubuti unafanyika ili ile formula inayotolewa iweze kuleta tija kwa wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba udhaifu umeonekana kwa samaki wetu wanaofugwa hasa hao tilapia ambapo kutokana na chakula wanacholishwa wanachukua muda mrefu lakini ukuaji wao wa kuweza kufikia nusu kilo na sentimeta 50 ili waweze kuvuliwa umekuwa sio wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili la ufugaji wa samaki kwa maana ya aqua culture katika nchi yetu ni jipya. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, sasa tunayo Kurugenzi mahsusi kabisa inayohusika na jambo hili la aqua culture na kupitia tafiti zetu mbalimbali za TAFIRI na vyuo vyetu vingine tunafanya jitihada za kuhakikisha tunaondoa tatizo hili la chakula cha mifugo hii ya samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wafugaji wote wa samaki nchini kwamba, baada ya muda siyo mrefu watafiti wetu hawa watabaini na kugundua lishe iliyo bora zaidi ili kuweza kukidhi mahitaji ya soko na mahitaji ya wafugaji wetu. Waendelee kujiandaa na kuendelea kuhamasishana katika ufugaji wa samaki, tatizo la chakula cha mifugo hii ya samaki litakwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pale kwenye Mji wetu wa Musoma tatizo la nyumba za polisi limekuwa ni tatizo kubwa na kwa muda mrefu. Na ninakumbuka kuanzia mwaka 2006 nimekuwa nikipiga kelele hapa Bungeni na bahati nzuri Serikali yetu sikivu ikakubali na ikaanza kujenga pale jengo na kufikia mwaka 2014 likawa limekamilika zaidi ya asilimia 85, lakini cha ajabu Serikali imeshindwa kutoa fedha za kulimalizia, matokeo yake wameanza kuiba milango, masinki na vitu vingine.
Je, Serikali sasa ni lini itatoa fedha ili ujenzi huu uweze kumalizika na wale askari waweze kuihsi vizuri?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru babu yangu Mheshimiwa Veda Mathayo kwa swali lake alilolileta. Nilishafika kwenye jengo hilo analoliongelea na kwa kweli limeshakamilika kwa kiwango kikubwa. Na sisi kama Wizara tunajipanga kuhakikisha kwamba, katika mwaka wa fedha huu fedha zitakazopatikana na ambazo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa majengo ambayo yameshafikia hatua nzuri, likiwepo hilo pamoja na maeneo mengine yanakamilishwa.
Kwa hiyo, punde fedha zitakapopatikana tutatoa kipaumbele kwa majengo haya ambayo yameshafikia hatua nzuri, ili yaweze kukamilishwa na askari waweze kuhamia. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi niweze kusema kuuliza swali moja la nyongeza.
Tunatambua kwamba katika kupambana na uvuvi haramu hawa Beach Management Units wamekuwa wakisaidia sana, lakini kwa bahati mbaya sana walikuwa hapati kipato cha moja kwa moja, kwa hiyo wakati mwingine wanageuka wao nao kushiriki katika uvuvi haramu.
Je, ni lini Serikali itaanzisha huu ufugaji wa samaki kwa njia ya cage ambao utakuwa unawapatia vile vikundi wa Beach Management Units kipato cha ziada ili waendelee kutunza maeneo yetu haya ya Uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue kwanza nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mathayo kwa sababu amekuwa mmoja kati ya Wabunge ambao wamejitahidi sana kuhakikisha kwamba wavuvi wao wanaingia katika ufugaji wa samaki vilevile uvuvi ambao ni endelevu, tunatambua jithata hizo zimezaa matokeo mazuri sana kwani katika eneo analotoka uvuvi haramu umepungua sana. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ufugaji wa samaki kwenye vizimba (cage culture) ni moja kati ya aina ufugaji wa sasa ambao Serikali imeamua kuhimiza wananchi wajihusishe nao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inachofanya ni kutoa elimu pamoja na kuweka mazigira wezeshi ambayo wavuvi mbalimbali wanaweza wakajihusisha katika cage culture kwa hiyo katika BMUs lakini vilevile kwa wavuvi mmoja mmoja kama kuna ambao wanataka kuingia katika ufugaji wa samaki katika vizimba Wizara yangu iko tayari kushirikiana na Halmashauri wanazotoka ili kutoa elimu ya njia sahihi ya kuweza kufanya ufugaji wa samaki kwenye vizimba.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri analifahamu vizuri suala hili la Kiwanda cha Nguo cha MUTEX, wale watumishi ajira yao ilikoma toka mwaka 1984 na baadhi yao mafao waliyopaswa kulipwa ilikuwa ni zaidi ya Sh.400,000 ambazo wao walizikaa kwamba hayo mafao yalikuwa ni madogo. Tumehangaika na suala hilo kwa kusaidiana na Mheshimiwa Waziri na hatimaye Desemba mafao yao yakatoka badala ya kulipwa zaidi ya Sh.400,000 wamelipwa chini ya Sh.100,000. Kwa sababu suala hili limechukua muda mrefu sasa, je, Mheshimiwa Naibu Waziri sasa yupo tayari kufuatana nami twende tukakae na hawa watumishi ili hilo suala liweze kuisha?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ameomba kuogozana nami kwenda Musoma Mjini, naomba nimwambie baada ya Bunge hili kuahirishwa ziara yangu ya kwanza ni kwenda Msoma Mjini kukutana na wastaafu hawa.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ningependa kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili wale vijana wanaoishi kando kando wa ziwa waweze kuona umuhimu wa kutunza ziwa lao na kuzuia uvuvi haramu. Ni lini sasa Serikali itaweza kutenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia kujenga mabwawa kando kando ya ziwa pamoja na cage ziwani ili ziweze kuwasaidi hao vijana katika kujipatia kipato ili waweze kuona umuhimu wa kutunza ziwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kila moja amekuwa akishuhudia akina mama wengi wanao nunua samaki wakiwa wamenyanganywa kwenye madishi yao, hata wale waliokaanga samaki wao wanaouza sokoni ambayo hii kusema kweli wao si wavuvi, lakini wanakuja kunyang’anywa samaki wale ambao wameshawanunua. Waziri anatoa kauli gani kuhusiana na unyanyasaji huu ambao unandelea katika baadhi ya maeneo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, mkakati wa Serikali tulionao wa kuhakikisha tunapunguza nguvu ya uvuvi katika maziwa na kuepusha vijana na uvuvi haramu katika kuhamasisha kufanya ufugaji wa samaki; tunaomkakati sana. Hivi sasa ninavyozungumza, tumeshaanza mkakati huo katika Ziwa Victoria ambapo wako watu binafsi walioanza ufugaji wa samaki katika vizimba lakini vilevile na sisi kama Serikali tumejiandaa kuhakikisha tunatengeneza incubators, kwa maana ya vikundi vya vijana ambavyo vitakwenda kufanya shughuli ya utengenezaji wa mabwawa lakini vilevile utengenezaji wa cages kwa ajili ya ufugaji wa samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Manyinyi ahakikishe anawaunganisha vijana wake kama nilivyotangulia kujibu katika swali la awali, wakae katika vikundi vya ushirika, nasi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tuko tayari kwenda kutoa elimu, lakini vilevile utaalam na kuhakikisha tunawasaidia vijana hawa kuwaongoza katika kufikia lengo sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni juu ya kauli gani tunatoa kwa ajili ya wale akina mama na wanawake wanaouza samaki katika mabeseni. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa tunalinda rasilimali za uvuvi. Katika lengo hilo, hatuko tayari kuona mwanamama anayefanya biashara ya uuzaji wa samaki katika mabeseni huko masokoni, anaonewa. Kama yuko Afisa wa Serikali anayekwenda kumsumbua na kumnyanyasa mwanamke anayeuza mafungu yake matatu, manne sokoni ya samaki, hii leo natoa kauli hapa katika Bunge hili Tukufu, jambo hilo ni marufuku. Kwa sababu lengo letu siyo kuangalia hawa samaki wanaowekwa katika mabeseni, lengo letu ni kutazama hasa kiini cha makosa haya yanayotokana na uvunjaji wa Sheria ya Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niwahakikishie tu akinamama wanaouza samaki nchini kote, wawe huru katika uuzaji wa samaki wao, wahakikishe kuwa wanapata kipato cha familia zao na kujenga Taifa letu.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika marekebisho ya Uwanja wa Ndege wa Musoma, nakumbuka Mheshimiwa Rais amefika pale mara mbili na mara zote ameahidi uwanja huo ujengwe kwa kiwango cha lami na uthamini umefanyika, sasa ni zaidi ya miezi sita. Nataka kupata kauli ya Serikali baada ya kuwa kuna sintofahamu, je, mpango wa kujenga uwanja huo upo au haupo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Manyinyi, Mbunge wa Musoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Ndege wa Musoma uko kwenye mipango ya kupanuliwa na kuwekewa runway kwa kiwango cha lami na TAA. Hivi karibuni nilifanya ziara Mjini Musoma tukakuta kuna changamoto ya fidia ambapo kulikuwa kuna mvutano wa hapa na pale lakini kuna timu ya wataalam imetumwa pale kwa ajili ya kwenda kuhakikisha ile changamoto ya fidia ya shilingi bilioni tatu na milioni mia saba inatatuliwa ili tuweze kulipa fidia na upanuzi uweze kuendelea.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, mkwe wangu, kwa majibu mazuri aliyoweza kunipatia, lakini (a) kwa kuwa Serikali imekiri kwamba kati ya watumishi 15,000 walioondolewa waligundua kwamba watumishi 4,160 waliondolewa kimakosa. Hawa ni wale waliopata nafasi ya kuja Dodoma, Utumishi na kwenda Dar es Salaam kwenye Tume. Wale ambao hawakuwa na uwezo, tafsiri yake ni kwamba wamebaki huko.

Sasa swali; ni lini sasa Serikali itaunda tume ambayo angalau itakwenda kila Halmashauri au Mkoani pale iwaite wale wote waliokumbwa na mkasa huu wa kupoteza ajira waje ili vyeti vyao viweze kuhakikiwa ili wale ambao hawakupata nafasi ya kuja waweze kurudi kazini?

Swali la pili; tunatambua kwamba wako watumishi ambao wamekaa au wametumikia nchi hii katika kipindi kirefu na wengine walibakiza tu mwaka mmoja wastaafu na kwa bahati mbaya wamekumbwa na huo mkasa; Serikali ina mpango gani angalau hata kuwapa kifuta machozi ili waende wakaanze maisha yao huko waliko kuliko kuwaacha kama ilivyowaacha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia sana suala la watumishi wa Umma, hususan wale ambao walikuwa wameandika taarifa zisizokuwa na ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kujibu swali lake la kwanza; kwanza kabisa naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge na kwa faida ya Watanzania wengine na Watumishi wa Umma wote kwamba Serikali ilishafanya zoezi la ufuatiliaji kwa zaidi ya asilimia 95 na hilo zoezi limeshakamilika. Wale watumishi wote ambao waliandika taarifa zao siyo sahihi katika personal records au kwenye OPRAS, naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba kama walidanganya watakosa stahiki zao zote kwa sababu Kanuni ya Utumishi wa Umma, kile kifungu D.12 kinasema mtumishi yeyote ambaye anaandika taarifa za uongo hataruhusiwa kuwa Mtumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali pia ilitoa msamaha hadi tarehe 31 Desemba, 2017, kwamba wale wote ambao walikuwa wamejiendeleza, basi walete taaifa zao kwenye Ofisi yetu ya Utumishi maana ilishatoa msamaha ili taarifa zao ziweze kuingia na waweze kurudi kazini. Kwa hiyo, zaidi ya watumishi 500 wamesharejeshwa na wale ambao walijiendeleza baada ya muda huo basi waweze kutuletea vyetu vyao tuweze kuhakiki na waweze kurudi kazini. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, ni kwa nini sasa hawa viongozi ambao mara kwa mara maana huwa tunashuhudia, kiongozi akifika mahali wanawapiga wakinyanyua mabango yao, wanapigwa, wanafukuzwa na kwa tamko hilo sasa ni kwa nini hawa viongozi wanaofanya mambo haya ya kunyanyasa wananchi wasichukuliwe hatua za kinidhamu?

Mhshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; mara nyingi huu utaratibu wa kutatua kero za wananchi, unakuta hata leo mfano Waziri wa TAMISEMI akifika pale ziko kero nyingi za wananchi yeye ndio anazitatua, au Waziri wa Ardhi akifika pale zinaonekana ziko wazi ambazo labda Mkurugenzi angeweza kuzitatua, lakini ameshindwa kuzitatua mpaka kiongozi afike pale. Hali hii sasa inaonesha dhahiri kwamba, leo baadhi ya kero nyingi zinaweza kutatuliwa tu pale ambapo viongozi wa Kiserikali au viongozi wakuu wanaenda pale. Serikali inao mpango gani wa kuhakikisha kwamba, hayo matatizo yanaisha na matatizo ya wananchi yanatatuliwa kule kwenye ngazi za wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge wa Musoma Mjini, ndugu yangu, kaka yangu Vedastus Mathayo Manyinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anataka kujua ni kwa nini kuna baadhi ya watu wanazuia wananchi kutoa kero zao au kuonesha mabango ambayo yamejaa hisia za changamoto zao katika maeneo yao na amesema kwamba, wanapigwa. Tunachojua ni kwamba, Mheshimiwa Rais na viongozi wengine wakifanya ziara wamekuwa wakiruhusu maswali kujibiwa na wananchi kutoa kero zao. Tukumbushane kwamba, pia kwenye mikutano ile ambayo kiongozi hasa Mheshimiwa Rais anapokuwepo ni mkusanyiko mkubwa sana. Sasa wakati mwingine ni watu wa usalama wanaangalia mazingira yalivyo, bahati mbaya sana yale mabango hayaratibiwi, kwa hiyo, wao wanachukua tahadhari kwanza ya kiusalama halafu wakigundua kwamba, ni ya hoja genuine, wana lengo la kupeleka kero, inaruhusiwa na wamekuwa wakifanya mara kadhaa tumeshuhudia sisi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nitoe wito kwamba, viongozi wetu hawa kwenye maeneo yetu ya mikoa na wilaya, tunao ugatuzi wa madaraka katika nchi hii kutoka ngazi ya kitongoji mpaka ngazi ya kitaifa na hii itaenda sambamba na kujibu swali lake la msingi, kimsingi Mheshimiwa Rais ameshatoa maelekezo, tumeeleza kwamba, viongozi wetu watoke ofisini, kama ni Mkuu wa Mkoa awe na utaratibnu wa kusikiliza wananchi wake katika eneo lake husika. Kwanza akutane na Wakuu wa Wilaya kwenye mkoa wake husika na watendaji wake, anapokea changamoto katika mkoa wake, wanaweka mikakati namna ya kutatua zile changamoto, halafu badae anafanya ziara kwenda kusaidia yale ambayo yameshindikana ngazi ya wilaya wasaidiane kama mkoa kuyamaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi maana yake ni kwamba, jambo ambalo lipo kwenye ngazi ya kitongoji limalizwe na viongozi wa kitongoji kwa tatizo husika. Jambo likitoka kwenye kitongoji kuja kwenye kijiji au mtaa liwe na uwezo huo walimalize, kwenye kata vivyo hivyo na kwenye ngazi ya wilaya na mkoa. Tukifanya kazi kwa pamoja kila mtu akaenda site, watu wasikilizwe, kero zitatuliwe, hakuna sababu ambayo itakuwepo tena Mheshimiwa Rais au Viongozi wa Kitaifa Mawaziri kwenda mahali mbalimbali kutatua kero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nitoe wito kwa viongozi wetu kimsingi ni kuonesha kwamba, mtu huyo kwenye mkoa au kwenye kata ameshindwa kufanya kazi. Kama kuna changamoto inatolewa mbele kiongozi wa Kitaifa akiwa kwenye ziara wakati pale kuna mtu ambaye ni wa kisiasa mwakilishi, lakini pia kuna mtu ambaye ni mteuliwa wa Rais au mamlaka nyingine halafu kuna watendaji wa Serikali. Tukifanya kazi kila mtu kwa ngazi yake hii habari ya kupeana mabango wakati viongozi wamekuja haitakuwepo, tutakutana na viongozi watafanya mambo ya jumla makubwa ya Kitaifa na tutaenda na maendeleo yetu kama kawaida. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba kabla barabara hazijajengwa tunatengeneza bajeti, tukishaipitisha ndiyo inaanza kutekelezwa. Wakati mwingine kuna miradi ambayo inatokana na majanga, mfano barabara imekatika ghafla na yenyewe haikuwa imetengewa fedha, lakini kila ukiomba fedha inakuwa ni maneno tu wala hazipatikani.

Sasa nataka kufahamu, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba tunapopata majanga kama madaraja yanapokatika, wa kutoa fedha za dharura ili kuyajenga kuliko hivi ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ujenzi wa barabara zetu unatekelezwa kwa mujibu wa bajeti za Serikali. Pia unatekelezwa kwa mujibu wa mapato yanayopatikana kutokana na makusanyo mbalimbali ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu wa kutenga bajeti na kuandaa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo lakini pia utayari wa Serikali kuhudumia majanga pale yanapojitokeza na kukata mawasiliano ni jambo ambalo linapewa kipaumbele sana na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba ni kupata taarifa rasmi kutoka katika jimbo lake kwa hiyo barabara na daraja husika ili wataalam wa TARURA katika eneo husika na ngazi ya Wizara tuweze kuona namna ya kufanya thamini na usanifu na kutafuta fedha kwa ajili ya kwenda kufanya ujenzi na marekebisho ya daraja husika.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana Mheshimiwa Waziri wa Nishati alikuja Musoma, na ninamshukuru kwamba tulienda naye pale kwenye Kata ya Bweli, Mtaa wa Bukoba tukaweza kuwasha umeme, na baada ya hapo tukaenda kwenye mkutano wa hadhara akaahidi kwamba sasa maeneo yote ya Musoma Mjini wataweza kupata umeme kwa gharama ya 27,000.

Hata hivyo, kila wananchi walipojaribu kwenda kulipia wanaambiwa mpaka waraka utoke kwa sababu haujapatikana. Sasa napenda kujua ni lini Mheshimiwa Waziri wa Nishati atatoa waraka ili wale wananchi wangu wa Jimbo la Musoma waweze kupata umeme kwa gharama nafuu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Manyinyi, Mbunge wa Musoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri kabisa kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yaliyotolewa yanatakiwa kuzingatia na kusimamiwa kama ilivyo na kwa kuwa tumesikia kuna lalamiko la namna hiyo, naomba tulichukue na tutahakikisha kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yanafanyiwa kazi kama ilivyoelekezwa, hakuna kupindisha maelekezo yaliyotolewa.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Mheshimwa Naibu Waziri maswalli mawili ya nyongeza pamoja na majibu mazuri aliyoyatoa. Swali la kwanza; ni ukweli usiopingika kwamba kama alivyosema ziko pikipiki ambazo labda wakati mwingine zinaokotwa na zinapelekwa pale. Kwa maana yake ni kwamba hakuna jalada lolote llinalofunguliwa kwenda mahakamani na matokeo yake pikipiki na magari kama hayo yanaweza kukaa zaidi ya miaka kumi.

Je, tunakubaliana kwamba sasa viendelee kukaa hapo na kuozea hapo au ni vizuri vikafanyiwa utaratibu mwingine ili hiyo fedha ikapatikana kwa ajili ya maendeleo ya nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wakati tunaunda Sheria ya kuruhusu bodaboda ili waweze kufanya kazi na kupata ajira kilichotokea ni kwamba zilezile faini zilizokuwa zinatumika kwenye vyombo vya usafiri ndio zilizochukuliwa na wakaanza kubandikwa bodaboda, lakini ikumbukwe kwamba bodaboda anabeba abiria mmoja, akikutwa na kosa analipa Shilingi elfu thelathini basi lenye abiria 60 akikutwa na kosa hilo hilo analipa elfu thelathini. Sasa napenda kujua ni lini Serikali itabadili hizi adhabu inayolingana na bodaboda ambayo ni ya chini ukilinganisha na adhabu iliyopo ambayo pia inatozwa kwa magari?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vedastus M. Manyinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameulizia, je, Serikali haioni haja ya bodaboda hizi ambazo zimelundikana katika vituo hivyo vya polisi basi ziuzwe au zipigwe mnada ili sasa Serikali iweze kujipatia mapato? Jibu ni kwamba, uwepo wa pikipiki hizi kwenye vituo hivi kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kutokana na sababu tofauti. Ukiziona pikipiki zimekaa kwenye Kituo cha Polisi usifikirie kwamba zimekaa kwa muda mrefu kwa sababu, utaratibu ni kwamba baada ya miezi sita endapo mwenye pikipiki yake asipokwenda kwenda kuikomboa pikipiki ama kulipa faini au taratibu nyingine akaziruhusu zikaendelea, maana pikipiki ile itaendelea kubakia pale.

Mheshimiwa Spika, baada ya miezi sita itaenda kupigwa mnada. Kwa hiyo inawezekana pikipiki hizo ambazo mnaziona kwenye Vituo vya Polisi ni kutokana na kwamba muda wake haujafika. Kwa mujibu wa taratibu hatutaweza kuipiga mnada ama kuiuza pikipiki ya mtu bila ya muda uliokusudiwa ama uliowekwa katika utaratibu kuwa haujafika.

Mheshimiwa Spika, utaratibu upo na kanuni na sheria zipo; ukiangalia kwenye PGO, ile 304 ukiangalia kwenye kifungu cha (1), (2), (3), (4), (5) na kuendelea imeelezwa Jeshi la Polisi limepewa mandate au limepewa mamlaka ya kuuza na kupiga mnada endapo itazidi zaidi ya miezi sita. Kwa hiyo hizo pikipiki zilizopo huko ni kwa sababu muda wake wa kufanyiwa hivyo haujafika, utakapofika hazitaonekana hizo. Aidha, nipende kusema kwamba tuendelee kushirikiana kutoa elimu huko kwa vijana wetu ili wasiendelee kuzifikisha huko.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa swali la pili, anasema, basi litapakia watu zaidi ya 30 faini yake ni Shilingi elfu thelathini, bodoboda ambayo inapakia mtu moja faini yake ni Shilingi elfu thelathini; sasa Serikali haioni haja hapa sasa ya kufanya marekebisho? Serikali katika hili bado haijaona haya ya kufanya marekebisho ya hili. The way itakavyofanya marekebisho kwa sababu nilivyomfahamu Mheshimiwa tushushe, maana kama basi watatoa shilingi 80,000, maana yake bodaboda watoe shilingi 10,000.

Mheshimiwa Spika, hizi Shilingi elfu thelathini ambazo zimewekwa bado matukio yanaongozeka na lengo letu sio kuwakomoa wananchi ama kuwakomoa vijana watumiaji wa bodaboda na pikipiki, lengo ni watu kufuata sheria kuepuka na kupunguza idadi ya ajali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka kufika Disemba, 2020 ajali za bodaboda ni 164; waliokufa ni 134 ambao wamekuwa injured 129 tu, tukizipunguza hizi tukisema sasa tuweke shilingi elfu kumi, vijana watazidi kufanya zaidi na hapo lengo na madhumuni ana uwezo wa kulipa Shilingi elfu kumi. Kwa hiyo tu niseme hatufanyi hayo kwa ajili ya kuwakomoa, tunafanya ili watu wafuate.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna utaratibu, nimekuwa nauona sana kule Zanzibar, vijana wanajazana kwenye magari makubwa yanaitwa mafuso, wanakwenda ufukweni huko muda wanaorudi huko wanarudi na bodaboda pikipiki hazipungui 30 au 40 njiani, lazima ajali inatokea, sasa kwa sababu analipa shilingi elfu kumi watafanya vyovyote kwa hiyo.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba tunayachukua mawazo tutakapo ona haja ya kufanya mabadiliko ya hii sheria tutafanya lakini kwa sasa naomba tuwe na hili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona na mimi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kile Kiwanda cha MUTEX, Mheshimiwa Naibu Waziri amekubali kwamba aliyekuwa anakiendesha alinyang’anywa kwa sababu alikuwa hakiendeshi kwa tija na sasa yapata ni miaka mitatu kile kiwanda kimesimama.

Je, ni kwanini basi hata huyo, huyo asingepewa akakiendeleza kuliko ambavyo sasa kile kiwanda kimesimama na watu wanakosa ajira?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa ubinafsishaji wa viwanda hivi kulikuwa na mikataba na katika mikataba hiyo kulikuwa na vigezo maalum na ndiyo maana tuliona sasa katika kuvunjwa kwa mikataba hiyo ndiyo maana imechukua muda mrefu ili kujihakikishia, ilikuwa mojawapo ni kumshawishi yule aliyepo kuona kama anaweza kuendeleza, lakini baada ya kujiridhisha kwamba ameshindwa ndiyo maana vimerejeshwa Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo ni kupata wawekezaji mahiri ambao kweli wapo makini na watawekeza kwa tija. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, kwanza tuna dhamira ya dhati ya kupata wawekezaji sasa mahiri ambao watawekeza katika viwanda hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tusingependa kuwaonea au kumpa mtu kwa upendeleo. Kwa hiyo tufuate utaratibu ambao utatangazwa na baadaye wawekezaji wengi watapatikana ambao watawekeza kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikia hapo Mheshimiwa Naibu Waziri ameweza kuonesha programu mbalimbali na nyingi ambazo Serikali inaendelea kuzifanya kwa ajili ya kuwasaidia vijana. Sasa wanasema wakati mwingine kuona ni kuamini. Hebu anieleze sasa: Ni lini Serikali walau itaanzisha hata programu moja katika Jimbo langu ili vijana wangu nao waweze kuona haya mengi ambayo Serikali imeweza kuyazungumza? (Makofi)

Swali la pili; kwa kuwa vijana wanaopata umri wa miaka 18 kwenda juu wapo wengi; na mojawapo ya jukumu kubwa la Serikali ni kuhakikisha kwamba vijana wanapata ajira: Je, ni kwa nini sasa Serikali isiwe na ule utaratibu kama iliyokuwa nao wa JKT wa crash programe ya miaka miwili au mitatu huko huko wanajifunza ukakamavu, kilimo, ufugaji wa samaki na mafunzo mbalimbali ili baada ya hapo Serikali iwape mitaji waweze kuendelea na maisha yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza kumshukuru sana Mheshimiwa Mbunge Vedastus Mathayo Manyinyi kwa namna anavyojitolea katika kuhakikisha vijana katika Jimbo lake na nchi yetu wananufaika na progamu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda kumhakikishia na kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Serikali kupitia bajeti ambayo mmetupitishia ambayo itaenda kutekelezwa kuanzia mwezi wa Saba mwaka huu tutapeleka programu ya greenhouse katika mikoa tisa iliyobakia ikiwemo Mkoa wa Mara na tutajenga greenhouse hizi katika kila Halmashauri. Kwa hiyo na Musoma Mjini ambapo anatoka kaka yangu Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi itapata greenhouse hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile programu hizo za uanagenzi tutafanya na vyuo mbalimbali vilivyopo Mkoa wa Mara ikiwemo Chuo kile cha Lake Victoria na vyuo vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kufanya kazi kwa ukaribu sana na wenzetu wa JKT. Utakumbuka pia katika wasilisho la bajeti la Wizara ambayo inahusika na masuala haya ya JKT, Waheshimiwa Wabunge tulipokea ushauri wenu kwa kuona namna ambavyo JKT inaweza ikatusaidia katika kuwajenga vijana na kuwaandaa kikamilifu ili waweze kujiajiri na kuajiriwa na hata kuajiri wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. Ahsante. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa pale Musoma Mjini hatuna Hospitali ya Wilaya na nimekuwa nikiomba mara nyingi Serikali iweze kutukabidhi ile hospitali iliyopo ambayo ni ya Mkoa na imeahidi kwa muda mrefu.

Napenda kujua ni lini sasa rasmi Serikali itatukabidhi ile hospitali iwe Hospitali ya Manispaa ya Musoma ili huduma bora zaidi ziweze kupatikana kwa watu wetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo nimesema ni tarehe 12 Disemba, 2022 wanaanza kuhama kwenda kwenye hospitali mpya halafu mnakabidhiwa Hospitali ya Wilaya na ibaki kutumika namna hiyo.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Katika nchi yetu kati ya matatizo makubwa tuliyonayo ni tatizo la ajira hasa kwa vijana wetu na tunatambua kabisa kwamba Wizara ya Kilimo ndiyo inayoweza kupunguza tatizo hili.

Je, Mheshimiwa Waziri umejipangaje katika WIzara yako kuhakikisha kwamba kilimo kinasaidia kupunguza ajira hasa kwa vijana wetu? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Manyinyi Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sekta ya kilimo ni sekta ambayo kweli inaweza kuajiri watu wengi sana lakini yapo mambo makubwa manne ambayo kwa muda mrefu yamewafanya vijana kutokuwa tayari kwenda kwenye sekta ya kilimo:

(i) Upatikanaji wa ardhi,
(ii) Upatikanaji wa mitaji,
(iii) teknolojia, na
(iv) soko la uhakika.

Mheshimiwa Spika, hii imewafanya vijana wengi kutokwenda huko. Kwa hiyo, kama Wizara tutakapokuja kusoma bajeti mwaka huu mtaona tuna-launch kitu tunaita ‘building a better tomorrow’ na tutaitengea fedha katika bajeti.

Mheshimiwa Spika, tunaanzisha block farm system ambako Serikali itachukua maeneo makubwa itayasafisha, itapima afya ya udongo, tutagawa block farm na kuwamilikisha vijana hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, kama ni eneo linahitaji fidia tutalipa sisi na yale maeneo yatakuwa owned na hao vijana ambao watakuwepo hapo na kuwaunganisha moja kwa moja na soko na kuijua afya ya udongo na mazao yatakayozalishwa kwenye eneo hilo. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Ni ukweli usiopingika kwamba Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi imepeleka fedha nyingi sana za kujenga vyumba vya madarasa na sasa watoto wote wanaenda mashuleni. Hata hivyo bado kuna tatizo kubwa sana la nyumba za Walimu. Je, ni lini sasa Serikali itakuja na mkakati thabiti wa kuhakikisha kwamba kunakuiwa na nyumba za Walimu za kutosha ili vijana wetu waweze kusoma vizuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, Mbunge wa Jimbo la Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ndio maana kwa sasa Serikali katika mipango yake kila mahali ambapo tunapeleka shule, tunahakikisha tunajenga na nyumba za Walimu katika kila shule ambayo tunaianzisha. vile vile mikakati mingine tuliyo nayo ni pamoja na kutafuta fedha ili kusogeza huduma hiyo ya makazi kwa Walimu, lakini tumeziagiza halmashauri kutenga fedha katika bajeti zao za ndani kuhakikisha katika kila bajeti ya mwaka wanaweka fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Walimu. Ahsante sana.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ile stendi ya Musoma Mjini Manispaa kipindi kama hiki cha mvua huwa inabadilika badala kuwa stendi inakuwa sawasawa na zizi, kwa maana tope zinajaa. Kwa kuwa Serikali ilishaahidi kuijenga tangu mwaka 2020 ni lini hiyo stendi itajengwa ili na sisi watu wa Musoma tuweze kuwa na stendi nzuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Jimbo la Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba stendi ya Manispaa ya Musoma ni mbovu na Serikali imeshachukua hatua kwanza kwa kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Musoma kuandaa tathmini ya mahitaji ya gharama za ujenzi, lakini pia kuanza kutenga fdha kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kwamba kunapohitajika miundombinu muhimu kama hii lazima wafanye tathmini, waanze kutenga fedha za mapato ya ndani asilimia 40 au 60 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa miradi kama hii ili kuondoa changamoto kwa wananchi, ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja la nyongeza. Pale Mjini Musoma kuna Mwekezaji aliyenyang’anywa kiwanda cha MUTEX kwa sababu ufanisi wake haukuwa mzuri. Serikali ikaahidi kwamba ndani ya muda mfupi tutapata Mwekezaji mwingine.

Je, ni lini sasa huyo Mwekezaji atapatikana kwa sababu ni zaidi ya miaka mitatu toka mwekezaji yule aondolewe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali tunahamasisha uwekezaji katika maeneo tofauti tofauti lakini Mbunge atakubaliana na sisi kwamba tayari kuna wawekezaji wengi sana ambao wameshaanza kuingia hapa nchini baada ya maboresho ambayo tunayafanya.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa tuna zaidi ya wawekezaji wa miradi 294 ambao wanategemea kuwekeza katika maeneo mbalimbali na tunategemea zaidi ya Bilioni Nane, Dola za Kimarekani ambazo zitawekezwa katika miradi hiyo ambayo tunaamini itaenda kutoa zaidi ya ajira 60,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Musoma nao katika eneo hilo la Mheshimiwa Mbunge miradi hii pia kwa kuwa tunashirikiana nae tutawasiliana tuone namna gani ya kuvutia wawekezaji hawa ambao wameonesha nia ya kuwekeza hapa nchini, waweze kuwekeza katika eneo la Musoma. Nakushukuru sana.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bweri ni kati ya vituo vya afya vya kwanza cha kwanza kujengwa pale katika Manispaa ya Musoma lakini hakikukamilika na kimechakaa sana pamoja na kituo cha Makoko.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ili tuweze kuvimalizia vituo hivyo viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya ambavyo Mheshimiwa Mbunge amaevitaja, kituo cha Bweri na Makoko ni sehemu ya vituo ambavyo Serikali inaweka utaratibu mahsusi kwa ajili ya kutenga fedha na kuvikarabati, vile ambavyo miundombinu haijakamilika vinatengewa fedha kwa ajili ya ukarabati na kujenga majengo hayo. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, madereva wengi wa bodaboda hawana leseni kwa sababu ya gharama kubwa zinazotakiwa kwa ajili ya kupata leseni, na ndiyo maana wanaendesha pasipo kuwa na leseni. Sasa swali; kwa nini tusiweke utaratibu mzuri wa kuwafundisha pamoja kwa gharama nafuu ili waweze kufanya kazi hiyo kwa uzuri?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi Mathayo, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunapokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge kwamba katika baadhi ya maeneo ikiwemo kwenye jimbo lake, ameanzisha huo utaratibu, na sisi upande wa usalama wa raia tunaupokea.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwahamasisha maeneo mengine pia watumie utaratibu kama huu unaopendekezwa na Mbunge, kwamba wanapokuwa wengi katika chumba kimoja wakafundisha kwa gharama za chini, wakawekewa utaratibu nafuu wa kupata leseni zao ili kuepuka hao wanaokwepa kukata leseni kwa sababu ya gharama kubwa. Na bahati nzuri maeneo mengine wameruhusu kulipa leseni kidogo kidogo, kwa hiyo likifanyika hilo nadhani hakutakuwa na matatizo yoyote.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Victoria mwaka jana lilichafuka sana na likasababisha Samaki wengi wakafa hasa wale watu waliokuwa wametengeneza Vizimba wakapata hasara kubwa, Serikali ilipotuma wataalam waliweza kusema kwamba ni kwa sababu ya vinyesi vya mifugo kwa maana ya ng’ombe ndiyo vimesababisha hali hiyo imetokea, yale majibu hakuna yeyote aliyekubaliana nayo.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba hali hiyo haijitokezi tena ili wananchi wanaoishi Kanda ya Ziwa wasiendelee kupata hasara?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mathayo, Mbunge wa Musoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tulipata changamoto sana katika Ziwa Victoria, changamoto hii ilisababishwa na suala zima la mkondo wa Mto Mara ulikuwa unashuka kule, hili kama tulivyosema ni kwamba lengo letu ni kwamba hatuhitaji wananchi waweze kupata hasara na katika hili ndiyo maana msisitizo wetu mkubwa ulikuwa ni jinsi gani wananchi kupewa elimu ya utunzaji wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneno mbalimbali tulivyoona miongoni mwa changamoto kubwa inayotokea ni uhalibifu wa mazingira. Leo hii hatuzungumzii Ziwa Victoria peke yake hata Ziwa Babati hivi karibuni, unaona kwamba ongezeko la magugu maji. Ndiyo maana Ofisi ya Makamu Wa Rais, Muungano na Mazingira ilichokifanya ni nini hivi sasa? Ilichokifanya sasa hivi ni kuandika maandiko mengi kwa pamoja na siyo linalozungumzia suala la Ziwa Jipe peke yake lakini sasa hivi tuna suala zima la Ziwa Babati, na eneo lote la Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu letu ni kuona jinsi gani tutafanya tupate mbinu mbadala ya kuhakikisha maeneo haya yote tunayatunza kwa lengo la kuwasaidia wananchi na uchumi wao. Ahsante sana.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, kile Kituo cha Afya cha Bweri ni kituo cha muda mrefu, lakini kimeshindwa kwisha na kwa hiyo, wananchi wa eneo lile wanashindwa kupata huduma;

Je, ni lini Serikali itamalizia hicho kituo ili wananchi wapate huduma nzuri za kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo hiki cha Afya cha Bweri ili tuweze kumalizia, na kama haijatengwa tutaangalia katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, licha ya vifo vya watoto wachanga vilevile kuna tatizo kubwa la wazee kwa sababu hawana uwezo wa kulipa gharama na hata vile vitambulisho vinavyotolewa na Halmashauri wengi wa wazee huwa wanapata usumbufu.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa bima za afya kwa ajili ya wazee ili waendelee kupata huduma nzuri?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, suala hili la wazee kuwa na vitambulisho lakini hawapati huduma limekuwa likitokana na upungufu wa dawa na vifaa tiba ambapo hata Mbunge ni shahidi kwa sasa masuala ya upatikanaji wa dawa kwenye vituo vyetu umeongezeka. Kwa hiyo, hili sasa limeshatatuliwa kwa asilimia 78 kwenye vituo vyetu na hospitali zetu. Hivyo tutaendelea kuongeza mpaka zifike asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, pili, suala ambalo linaweza likatusaidia sisi kuondokana na hili tatizo moja kwa moja, ni sisi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba ni lazima twende kwenye suala la Muswada wa Bima kwa Wote na ndilo suluhisho la kudumu kwa hilo. Lakini wakati huo kabla hatujafikia kwenye suala la Bima ya Afya kwa Wote kuna utaratibu wa kwamba mtu/mzee anayeshindwa kulipa kabisa na anayepata shida tunaweza tukatumia kwa maana ya kupata barua na mambo mengine, lakini sheria zetu vilevile zinatoa room kwa watendaji wetu kuwaaandikia barua na kupata huduma.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Musoma Mjini, Mitaa kama Bukoba, Songambele, Zanzibar na kule Bukanga mwaka mmoja nyuma ilikuwa inapata umeme wa shilingi 27,000 kwa sababu ni mitaa ya pembezoni. Lakini kwa sasa hivi tayari mambo yamegeuka, wanalipa zaidi ya shilingi 300,000 ambapo wananchi wengi hawana uwezo.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu kuendelea kuwaruhusu waendelee kulipia umeme kwa bei ya shilingi 27,000 kama ilivyokuwa awali?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mathayo Manyinyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto ya tafsiri na utekelezaji wa gharama za kuunganisha umeme kwa wananchi, na kwa haraka haraka kuna watu wako maeneo ya mijini na wanaonekana wako mijini lakini hali zao za kiuchumi haziwezi kukidhi malipo ya gharama kubwa ya kuunganisha umeme. Lakini vilevile kuna watu wanaonekana wako maeneo ya vijijini, lakini hali zao za kiuchumi ni kubwa na wanaweza wakalipa zile gharama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuonekana kuna changamoto hiyo tumepata maelekezo kutoka kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, na tayari imeundwa timu ambayo inapita kila eneo na kubaini namna gani nzuri ya kuweza kupeleka umeme na gharama nafuu katika maeneo hayo. Na katika bajeti tunayosoma kesho hilo ni eneo mojawapo ambalo tutalieleza na kutoa ahadi njema ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pale Musoma Mjini tuna tatizo kubwa sana la ajira kwa sababu viwanda vingi vimekufa; vilikuwepo viwanda vya samaki vimekufa, Kiwanda cha Nguo cha MUTEX kimekufa, Kiwanda cha Maziwa kimekufa, Kiwanda cha Mkonge kimekufa. Sasa ni zaidi ya miaka kumi kila siku Serikali inaahidi kutafuta wawekezaji. Sasa tunapenda kujua, ni lini sasa itatusaidia kupata hawa wawekezaji ili watu wetu waendee kupata ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, napenda kujibu swali la nyongeza dogo la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama nilivyosema, tulipofanya tathmini ya mwaka 2017 kuhusiana na viwanda vilivyobinafsishwa, viwanda vingi zaidi ya 68 vilikuwa havifanyikazi vikiwemo viwanda ambavyo viko katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunge kule kule Musoma. Kama nilivyosema katika tathmini hiyo tumeshavigawa vingine tunavitafutia wawekezaji, lakini vingine tutaviweka katika mashirika maalum ikiwemo maeneo huru ya uzalishaji kwa ajili ya mauzo ya nje (SEZ), lakini vingine katika taasisi zetu kama Shirika la Maendeleo la Taifa – NDC na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, lakini katika kutafuta wawekezaji kuna hatua mbalimbali kwa sababu tusingependa kurudia tena makosa tuliyoyafanya huko nyuma kutafuta/kupata wawekezaji ambao siyo mahiri. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali inajitahidi kuhakikisha kuweka mazingira wezeshi, ili kuvutia wawekezaji ambao tunajua watakuwa ni makini na wenye nia thabiti ya kuvifufua au kujenga viwanda vingine ambavyo vitakuwa na tija kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii. Nakushukuru sana.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali dogo la nyongeza. Kila mwaka Serikali imekuwa ikiahidi kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia kituo cha afya cha Bweri. Sasa ni lini tutapata hizo fedha ili kile kituo kiweze kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bweri tayari kimeingizwa kwenye orodha ya vituo vya kimkakati ambavyo vinatafutiwa fedha kwa ajili ya ukamilishaji. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge awe mvumilivu, aamini kwamba Serikali ipo kazini na mara fedha itakapopatikana tutahakikisha kwamba tunaipeleka kwa ajili ya kukamilisha Kituo cha Afya cha Bweri. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya CCM inasema wazi, watoto chini ya miaka mitano matibabu ni bure. Akinamama wajawazito matibabu ni bure lakini kumekuwa na tatizo sugu la kuendelea kuchajiwa fedha; je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba hilo tatizo linaisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, hilo tatizo litaisha kwa sisi kushirikiana kwa pamoja. Kama ambavyo jana nilisema, miongozo na taratibu za Serikali ziko wazi, lakini inapofika kwenye vituo vyetu, zahanati zetu kule wilayani, watu hawafuati maelekezo ya Serikali; kwenye Serikali kwenye eneo husika, tunalo Baraza la Madiwani ambalo linatakiwa wakati wote kwenye mijadala yao wajadili na sehemu ya tiba na kuona watu wake kwenye eneo hilo wanahudumiwaje na Mkuu wa Wilaya kupitia Kamati ya Ulinzi na Usalama kufuatilia wakati wote na kuhakikisha haya maelekezo ya Serikali yanafuatwa vizuri.

Mheshimiwa Mbunge, tumekuja na Bima ya Afya kwa Wote. Ninakuomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane kwa pamoja inapofika wakati wa utekelezaji. Tushirikiane kwa pamoja kwa sababu tukishirikiana pamoja nakuhakikishia kwamba, tukienda kwenye Bima ya Afya kwa wote, hii migogoro yote itaenda kuisha na hatutaendelea kubishana kwa mambo madogo madogo kama haya.