Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mheshimiwa Rais kuwa na imani na mimi. Vilevile ndugu zangu wa Jimbo la Musoma Vijijini ambao waliamua niwe mwakilishi wao mzuri, tumeanza kujenga uchumi kwa kasi kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais ni agizo na Wizara ya Nishati na Madini imeanza kutekeleza kwa vitendo. Niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango mizuri na wengi ambao wamechangia watakubaliana name kwamba wengine nimeanza kutatua kero zao. Kwa hiyo, wengi wanaomba umeme. Nawathibitishia Watanzania kwamba unakuja umeme mwingi, wa uhakika na wa bei nafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wachimbaji wadogo wanatafuta maeneo, na watapewa na vilevile ruzuku itaendelea kupatikana. Tulianza na dola 50,000, tumefika dola 100,000 na tunataka tupate wachimbaji wadogo wanaoweza hata kufika kwenye ruzuku ya dola 1,000,000 au 5,000,000 hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, agizo la Mheshimiwa Rais, ni suala la kuondoa umaskini ambao unaendana na kujenga uchumi imara. Ni lazima uchumi wetu ukue kwa zaidi ya asilimia 10 na kufanya hivyo ni kila Mtanzania atumie umeme mwingi, aliyepo shambani na aliyeko kwenye viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi wastani wa matumizi ya umeme wetu, kila mtu hapa, hata tuliokaa humu ni unit 9 kwa mwezi. Kazi niliyopewa ni kuwatoa kwenye unit 9 kwa mwezi, kwenda kwenye unit 250 kwa mwezi. Hiyo ndiyo inayoitwa nchi ya kipato cha kati. Tukifanya hivyo, uchumi utakua kwa zaidi ya asilimia10 kutoka asilimia 7 za sasa hivi. Tukiendelea na asilimia 7 na asilimia 8 umasikini hautatoka.
Kwa hiyo, Wizara ya Nishati na Madini inataka ilete umeme mwingi. Tuna vijiji 15,809; asilimia 33 tu ya vijiji hivi ndiyo vyenye umeme. Kwa miaka miwili inayokuja, ni lazima tufike angalau asilimia angalau 67, theluthi mbili ya vijiji hivyo vipate umeme. Sasa hivi ni asilimia 40 ya Watanzania wote wanaopata umeme. Tukitaka kuingia nchi ya kipato cha kati, ikifika mwaka 2025 angalau asilimia 75 ya Watanzania na ikifika mwaka 2030 kwa sababu Tanzania ndiyo iliwakilisha Afrika kwenye mambo ya nishati duniani, ni lazima tuwe zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania wanaotumia umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutafanyaje sasa? Ni kutumia ni vyanzo vyote vya umeme ambavyo tunavyo. Kwa sasa hivi gesi ni karibu asilimia 50, maji asilimia 35 na umeme wa mafuta karibu asilimia 15. Ni lazima tuachane na umeme wa mafuta, uwe umekaa pale kama tahadhari yetu tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutazalisha umeme mwingi kutokana na gesi asilia, makaa ya mawe na maji. Halafu ndiyo tunakuja nishati jadidifu yaani jua, upepo na mengineyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kwasababu hesabu hizi lazima ziendane na muda. Leo hii Watanzania tuko milioni 53.5; tutakavyokuwa tunapiga kura mwaka 2020 tutakuwa karibu milioni 65; na tutakapofika mwaka 2025, tukiwa nchi isiyokuwa na maskini na mtu anaamua anachotaka kula, kama mimi napenda muhogo basi tutakuwa karibu watu milioni 80 na uchumi hapa ndugu yangu inabidi Pato la Taifa liwe zaidi ya shilingi bilioni 240 mwaka 2025. Kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania umeme wa uhakikia ni lazima. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Huu ni Mpango mzuri. Waheshimiwa Wabunge mawazo yenu tumeyapata na tutayafanyia kazi na mengine tunayafanyia kazi tayari. Cha maana cha kujua ni kwamba maana ya uchumi ambao unafanyiwa mapinduzi makubwa huwa mara nyingi haukubaliki kiurahisi, ndio historia ya mapinduzi ya kiuchumi duniani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa mafuta na gesi, nataka niwaeleze Watanzania ukweli, wengine wamesema hakuna wataalam siyo kweli na wala hatuhitaji kumleta kama alivyosema mwingine mzungu mmoja aje kutufundisha, haiwezekani hiyo. Kwa sababu huku kuna watalaam kweli kweli. TPDC penyewe kuna Ph.D nne, kuna Masters 62, kuna shahada za kwanza zaidi ya 200. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kina degree programmes zaidi ya tano, UDOM wapo tano, lengo ni kwamba kwa miaka michache inayokuja Tanzania ndiyo itakuwa na wataalam wengi wa madini na mafuta nchini hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunasomesha watu, mwaka huu Norway tumemaliza scholarship ya watu 40 na wengine 40 tutaziomba tena. Kwa hiyo, maana ya mageuzi haya tunayoyaongelea ndugu zangu Wabunge yataendana na uchumi wa gesi, ndiyo roho ya mapinduzi ya uchumi wetu na niwahakikishie tuko kwenye njia nzuri. Wanaosema hawaoni faida, umeme utatoka huko, viwanda vya mbolea tutajenga, majumbani tutatumia na gesi tutaisindika.
Mheshimwa Mwenyekiti, niongelee kingine ambacho ni injini ya mageuzi yote haya, ni mambo ya umeme. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote ni kwamba, umeme wa uhakika na umeme wa bei ndogo lazima utapatikana kwenye Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kwa mahesabu, sio kwa hisia, sio kwa matusi, sio kwa kumkejeli mtu. Ni lazima tutoke kwenye power per capita, yaani mtu mmoja mmoja, mwenye umeme wa units 108 kwenda units 3000. Ndio kazi ambayo Wizara ya Nishati inaifanya. Hiyo inaendana na ukuaji wa uchumi, utoke sasa hivi asilimia saba mpaka asilimia 10 kwa mwaka ili ifikapo mwaka 2025, tukiwa nchi ambayo ni ya kipato cha kati, yenye Pato la Taifa GDP ya bilioni 240, tunahitaji umeme wa uhakika na Wizara ya Nishati na Madini na Serikali kwa ujumla ndiyo kazi inayoifanya hiyo.
Sasa Waheshimiwa Wabunge kingine ambacho ni cha kufahamu, tumeongelea sana fedha za wafadhili, Watanzania wote naomba tuelewane, fedha za wafadhili ni tofauti na fedha za uwekezaji. Mimi huku Wizara ya Nishati na Madini, hata wakinipatia fedha zote za wafadhili, ni fedha kidogo. Fedha za wafadhili, wasiojua siyo zaidi ya dola milioni 500 kwa mwaka, dola za Marekani hazivuki milioni 500. Halafu upatikanaji wake, kwa ndani ya miaka 10 hesabu zimepigwa ni wachache wamevuka asilimia 50 ya ahadi walizozitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kinyerezi I, megawati 150, uwekezaji ni dola milioni 183. Kinyerezi II ambayo tutaweka jiwe la msingi mwezi huu, inahitaji dola za Marekani, milioni 344. Hizo ni zaidi ya fedha za wafadhili. Kwa hiyo, tunachokitafuta sisi, ni fedha za uwekezaji, kwa hiyo, Watanzania msiwe na wasiwasi, fedha za wawekezaji zitapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wamesema Exim Bank ya China imekataa, siyo kweli. President Jinping alivyokuwa Afrika ya Kusini ametoa dola bilioni 60, kwa uhusiano wa China na Afrika. Tanzania ni kati ya nchi tatu ambazo zitafaidika. Nawaambia Wizara yangu yenyewe, mimi nataka…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kutoa pongezi kwa Waziri wa Fedha, Naibu na Wizara nzima ya Fedha kwa sababu wametengeneza bajeti ambayo ni ya mwaka mmoja lakini iko kwenye picha ya miaka mitano na iko kwenye picha ya dira yetu ya maendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyojadili hii bajeti usiichukue kama ni ya mwaka mmoja, lazima uone kwamba ni bajeti ambayo imeanza safari ya kwenda mwaka 2025. Kwa hiyo ikiwa kweli tumedhamiria kuwa nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 inamaanisha bajeti yetu lazima inapanuka, inakuwa kubwa na fedha nyingi zinaenda kwenye maendeleo na siyo matumizi ya kawaida na ndiyo shukrani zangu nazitoa kwenye hii bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema tunataka kuwa nchi ya kipato cha kati mwaka 2025 maana yake ni kwamba ukipiga hesabu, bajeti yetu sasa hivi ni vizuri nikiongea kwenye dola kwa sababu nalinganisha na nchi zingine, GDP yetu (Pato la Taifa) karibu kwenye bilioni 55, 56. Kama tunataka kuwa nchi ya kipato cha kati, mwaka 2025 tunataka bajeti yetu ambayo itaonesha kwamba GDP per capita (pato la mtu mmoja) litakuwa la dola 3,000 inabidi tuizidishe mara nne. Kwa hiyo hii bajeti ni kubwa kwa sababu ifikapo mwaka 2025 tukiwa nchi ya kipato cha kati ni lazima tuwe na GDP ambayo ni zaidi ya bilioni 200 tuzidishe mara nne bajeti ya sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi engines ziko nyingi sana, engine za kupeleka vitu huko mbele huko na engine mojawapo ni umeme, na ndiyo maana bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini imekuwa kubwa ni ya shilingi trilioni 1.23 katika hiyo bajeti asilimia 94 zinaenda kwenye maendeleo na ukichukua kwenye maendeleo asilimia 98 inaenda kwenye umeme. Hapo ndipo unajua bajeti ya Serikali iliyotayarishwa na Dkt. Mpango na wenzake imedhamiria kweli kutufikisha uko. Dalili za kusema kwamba fedha zinapatikana ni kweli zitapatikana, mwaka huu tunaomaliza mwezi huu, Wizara ya Nishati na Madini upande wa maedeleo tumeshapata asilimia 82 na REA - umeme vijijini tumeshapata asilimia 81.
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti yetu kwa hiyo ni kwamba umeme vijijini ndiyo itawatoa watu kwenye umaskini. Bajeti mliyoipitisha ya umeme vijijini imo ndani ya bajeti kubwa ya Serikali ambayo ni ya umeme vijijini shilingi bilioni 534.4, hii imeongezwa kwa asilimia 50 ya bajeti ya mwaka uliopita. Lakini Waheshimiwa Wabunge na Watanzania ni kwamba kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchii hii, na kuonesha hii Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kujenga nchi ya viwanda, ni kwamba umeme vijijini tutakuja kufikisha trilioni moja. Kwa sababu hii ni Serikali inayoaminika, hata wenzetu wanaopenda kutuchangia maendeleo na wao wanaweza wakachangia zaidi ya bilioni 500 na taarifa nitawapatia ndani ya wiki mbili kutoka sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hii bajeti inahakikisha umeme unapatikana, siyo umeme tu kusambaza, lakini hii bajeti ndiyo itatuhahakikishia kwamba vyanzo vyetu vyote tulivyonavyo vya umeme tunaanza kuzalisha umeme. Tumejipanga kuzalisha umeme kutokana na gesi asilia, makaa ya mawe, maji, sola, upepo, joto ardhi, mawimbi (tides and waves) na mabaki ya mimiea (bio energies). Hayo yote yako kwenye hii bajeti ya trilioni 29.5, kwa hiyo ndugu zangu Wabunge tusipoipitisha hii, tukiwa na wasiwasi nayo basi haya yote ya umeme hayatakuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, na hii bajeti uzuri wake ndiyo inakuja kutuhakikishia kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchi hii haya mambo ya umeme ambao unakatikakatika hii bajeti ndiyo nakuja kutoa suluhisho la kudumu. Tunajenga njia za kusafirisha umeme kutoka kilovoti 220 tunakwenda kilovoti 400.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, mimi ningependa kuzidi kuwashawishi kwamba hii bajeti siyo ya mwaka mmoja bali inaanza safari ya kutufikisha mwaka 2025 na kwenye hii bajeti ndiyo tumeweka miradi mingi ya usambazaji wa umeme na ni muhimu sana. Waheshimiwa Wabunge wengi mmelalamika kwamba kuna vijiji vimerukwa. Hii bajeti ndiyo ina mradi wa kushusha transfoma na kusambaza nyaya kwenye vijiji ambavyo vimerukwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, mmesema hii sekta ya nishati haijashikwa vizuri sana na Watanzania. Hii bajeti ndiyoina fedha za kuwawezesha wazalishaji wadogo wa umeme na wao waweze kuchangia kwenye umeme wa Gridi ya Taifa. Vilevile kwa upande wa kuboresha upatikanaji wa umeme, hii bajeti itatuwezesha kuibadilisha TANESCO kabisa itoke TANESCO ya zamani kuja TANESCO ya karne ya 21. TANESCO itakuwa na ushindani, lakini bajeti ya kubadilisha muundo, mfumo na utendaji unaolalamikiwa wa TANESCO uko kwenye hii bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaoenda huko kuanzia tarehe 1 Julai tunaweka taratibu za kisheria za kunyang‟anya TANESCO mamlaka ya yenyewe ndiyo inazalisha peke yake, ndiyo inauza umeme peke yake, ndiyo inasafirisha umeme peke yake.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, mimi nigependa bado kusisitiza kwamba ni muhimu sana hii bajeti tukaiunga mkono na istoshe tumekuwa na sehemu tunaulizia ni kwamba kwa mfano wengine wamesema fedha za CAG, fedha za nani, ukweli ni kwamba bajeti hii acha ianze kufanya kazi na mahali ambapo tutakwama tutarudi tena hapa Bungeni kurekebisha.
Meshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo hii bajeti ni muhimu na diyo itatufikisha mwaka 2025 ambapo GDP per capita yetu ambayo itatoka sasa hivi dola 945 GDP per capita mpaka kwenda dola 3,000 kama GDP per capital.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe shukurani nyingi kwa Wabunge wote kwa sababu maswali yalikuwa ni mengi sana mliyoyauliza kwa kuongea na maswali mengi sana mmeyauliza kwa maandishi na ikifika saa mbili usiku leo, tutakuwa yote tumeyajibu na tumeya-bind kama hivi, mpaka wale waliouliza kabla hatujakwenda mapumziko tayari tumeshayajibu. Kwa hiyo, niombe kwa ruhusa yako jibu la kila mtu tutaliweka kwa maandishi na tutawasambazia Wabunge wote kupitia ofisi ya Bunge. Hiyo inaonesha jinsi ambavyo ufanisi ulivyo mkubwa kwenye Wizara ya Nishati na Madini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kutoa shukurani kwamba yote mliyoyasema tumeyazingatia na tutayafanyia kazi kwa sababu maswali yanafanana fanana na ushauri unafanana fanana, ni vizuri nijibu kwa pamoja na ili mpatemwelekeo wa Taifa linakwenda wapi. Kwanza nianze na suala la Zanzibar, ndugu zangu wa Zanzibar hakuna suala lingine tena kwa sababu sheria imeshawaruhusu mnaweza mkatafuta mafuta wenyewe na mkayaendeleza nyie wenyewe. Hakuna anayewagandamiza, lakini niwaeleze mambo sasa ya kitaalam kuhusiana na hayo mafuta. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala ambalo itabidi mkae na majirani zenu na ndiyo maana inabidi utafiti ufanyike, ijulikane mna gesi kiasi gani, mna mafuta kiasi gani na yako wapi. Hilo swali hilo, yako wapi? Huku upande wa Msumbiji na Tanzania itabidi Tanzania na Msumbiji tukae chini kwa sababu gesi ile na mafuta haikuheshimu mpaka wa Ruvuma. Ziwa Tanganyika itabidi tukae pamoja na Kongo kwa sababu mafuta na gesi iliyomo pale haijaheshimu ule mpaka wa katikati ya ziwa. Kwa hiyo, ni vizuri ndugu zangu kama nchi moja ni lazima kwanza tujue mafuta hayo na gesi iko wapi, geographic location, halafu tukitoka pale tunakwenda kwa wataalam wanaojua, kuna the law of the sea ambayo ina define continental shelf na margin ya kila nchi. Kwa hiyo niwaachie hapo, inabidi bado tushirikiane.
Mheshimiwa Naibu Spika, nije upande wa umeme, Naibu Waziri ameongelea, watu wanasema tuwe na vyanzo vingi. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania ni kwamba Wizara inavijua, imeshavipigia mahesabu na hiyo ndiyo inaitwa energy mix au energy matrix. Tunakuwa na uhakika wa umeme kupatikana kwa sababu tutazalisha umeme kutoka kwenye gesi asilia, kwenye makaa ya mawe na kwenye maporomoko. Tutazalisha umeme kutoka kwenye jua, kwenye upepo, kwenye joto ardhi, kwenye bio-energies yaani biomass na biogas. Umeme wa joto ardhi, tumetengeneza ramani Tanzania tunajua joto ardhi iko wapi na ndiyo maana tunataka kuanza kuchoronga pale Ziwa Ngozi, Mbeya. Tunachotafuta sasa hivi ni kujua ukubwa wa volume ya ile steam inaweza ikazungusha turbine ya ukubwa gani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaambie kwamba, vyanzo vipo, vinatosha na tunavifahamu. Hata speed ya upepo wa Singida tumeshapiga mahesabu, speed yake ni kali, ni mita tisa kwa sekunde moja ambayo inaruhusu kuweka mitambo ya kuzalisha umeme wa upepo na upande wa jua vile vile tumetengeneza ramani tunajua sehemu ambazo tunaweza tukapata umeme mwingi sehemu za Singida, Shinyanga na Dodoma. Kwa hiyo, kitaalam tuko vizuri tunajua kwamba umeme utapatikana wa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye suala la tunakokwenda. Haya mahesabu tukienda hatuendi kwa kubahatisha. Wizara hii ya Nishati na Madini ni lazima uchanganye sayansi, uchanganye na uchumi ndiyo utakwenda vizuri. Tumeshasema tuna maendeleo tunataka kuwa nchi ya kipato cha kati. Kuingia kwenye kipato cha kati kinaanzia dola 1,045, sisi tumesema tunataka kuanzia dola 3,000. Kwa hiyo, mwaka 2015 kama tutakuwa na GDP per capita ya dola 3,000 na sasa hivi GDP yetu ni karibu dola bilioni 50, iko inayumba yumba kidogo pale na tukichukulia kwamba tunazaliana kwa kiwango cha asilimia nne, kwa hiyo kufika mwaka 2025 huenda tutakuwa kati ya watu milioni 65 au milioni 70.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mahesabu tunachukulia milioni 70 ukipiga mahesabu ya GDP per capita 3,000 ni lazima GDP yetu iwe na bilioni zaidi ya 200, ndiyo linakuja suala la umeme sasa. Kuendesha huo uchumi unahitaji umeme mwingi na ndiyo maana unaona bajeti ya hii Wizara imejiwekeza kupatikana umeme mwingi, kwa hiyo ndugu zangu hivi vitu vinakwenda kwa mahesabu siyo kwa nadharia na ndiyo maana speech yangu ilikuwa imejaa takwimu, haikujaa malalamiko na matusi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu kwenye dunia ya sasa ni lazima tufanye biashara ya umeme. Ndiyo maana tunajenga huu msongo wa kilovolt 400 kutoka kwenye mpaka wa Zambia na kwenye mpaka wa Kenya. Tunataka kuuziana umeme, hakuna sababu wewe kununua umeme wa bei mbaya hapa wakati Ethiopia wana umeme wa bei nafuu, huko ndiko tunakokwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ethiopia na nchi za Afrika Mashariki, nchi 11 tumeshawekeana mkataba tutatumia umeme wa maji ambao ni senti saba kwa unit moja. Kwa hiyo, suala la kutumia umeme wa mafuta tena ni historia kwa hii nchi. Kwa nini mtu atuuzie umeme wa bei mbaya wakati transmission line tunatoa umeme Ethiopia kuja huku. Kwa hiyo, ndiyo maana ya kuweka hizi na ndiyo maana kila Jumapili umeme unakatika kwa sababu tunajenga msongo mkubwa wa kusafirisha umeme, ni heri uumie sasa upate faraja baadaye. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuendesha haya yote tunaitaka TANESCO mpya. Wengine wanasema TANESCO igawanywe imekuwa kubwa sana. Ndugu zangu kwenye dunia ya nishati, TANESCO ni kitu kidogo kabisa hamna kitu. Kwa sababu kama alivyosema Naibu Waziri, uwezo wetu wote wa umeme ni megawatts 1,500. Kampuni moja India inazalisha umeme na kuuza zaidi ya megawatts 100,000, sasa wewe utagawa kampuni yenye megawatts 1,500 unakuwa unagawana umaskini tu pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, watu wanaopata huduma ya TANESCO bado ni wachache. Kwa hiyo, mabadiliko ya TANESCO ni kwamba inakwenda yenyewe inajibadilisha na sehemu zingine za TANESCO zinazikwa, zinakufa, ndiyo maana sasa hivi uzalishaji wa umeme uko wazi, kuwa mtu yeyote anaweza kuzalisha umeme na anaweza akamuuzia mtu yoyote bila kupitia TANESCO.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ule mradi tunavyokwenda kufika mwaka 2025, kama ulivyo na simu ya tigo, ya voda, ya nini, TANESCO ya mwaka 2025 itakuwa ni hiyo hiyo. Unachagua nani akuuzie umeme kama ilivyo nchi zingine duniani na wote wamekwenda huko na wengine bahati nzuri wamekulia huko, kwa hiyo TANESCO inabadilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uwekezaji mpya nakiri kwamba kuna mikataba mibovu, sasa dawa yake tunatengeneza vigezo vya kuwekeza kuleta ushindani. Tarehe 30 hii document itakuwa tayari, itasambazwa dunia nzima na tutawaambia kwamba tunataka Lindi tunataka megawatt 300, je, wewe Kampuni hii unatupatia ofa ipi? Tunataka makampuni yashindane na hii itatoa haya mambo ya rushwa na mambo ya kupata mikataba mibaya. Kwa hiyo, ndugu zangu ngojeni tarehe 30 na kuonyesha kwamba sisi tuko wazi kabisa, World Bank, African Development Bank wote wamehusishwa kutengeneza hii document, ushindani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, usafirishaji ameshaueleza, usambazaji vile vile tunakokwenda ikiwa hawa wakandarasi wa REA wanasambaza umeme vijijini, kwa nini watu binafsi wasisambaze umeme badala ya kutegemea tu TANESCO? Ndiyo hiyo nasema mabadiliko TANESCO vile vile haitakuwa inasambaza umeme peke yake. Ndiyo mabadiliko hayo yanakuja na hii document siyo vitu vya kichwani tumeshaitayarisha, imeshapitishwa kwenye Cabinet.
Mheshimiwa Naibu Spika, deni la TANESCO, nakiri kwamba deni ni kubwa na upande mmoja ni mikataba mibovu, kuna wizi, kuna rushwa na uongozi dhaifu. Ndugu zangu Watanzania niwaeleze, mtu asije akaueleza ubora wa kampuni yoyote ambayo inauzia TANESCO umeme sasa hivi, haipo. Labda kama awe ametumwa kuishabikia lakini tukisema ukweli mbele ya Mwenyezi Mungu mikataba yote siyo mizuri. Sasa nimechukua hapa mifano, utasikia mwingine anaimba SONGAS, SYMBION. SONGAS capacity charge kwa mwezi tulikuwa tunawalipa dola za Marekani milioni nne nukta sita, SYMBION milioni mbili nukta nne, IPTL milioni mbili nukta sita, AGGREKO milioni mbili, hakuna ambayo ina manufaa makubwa kwetu. Kwa hiyo, ndugu zangu ninachowaomba Wabunge msitumiwe, msishabikie mkaja hapa kutetea Kampuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini uongozi wa TANESCO sasa hivi unabadilika, kila baada ya miezi mitatu tunafanya tathmini. Ukitaka kubaki Meneja wa TANESCO ni lazima kila baada ya miezi mitatu tukutathmini. Umekusanya fedha kiasi gani za Shirika? Umeunganisha wateja wapya kiasi gani? Umekuwa na ubunifu wa kutatua matatizo ya umeme kwenye eneo gani na kwa kiasi gani?. Tathmini ya pili inakuja tarehe 1 Juni, moja ilishafanyika watu wakaanguka, mwezi wa Sita tarehe moja inafanyika, tarehe 1 Septemba inafanyika. Kwa hiyo, kila miezi mitatu. Kwa hiyo, ukitaka kuwa Meneja TANESCO inabidi ujitume kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nguzo. Ni kweli kwamba nguzo tumesema TANESCO haipaswi kum-charge mtu. Ni tatizo la ukosefu wa fedha, tunakubali hilo lakini ni suala la mpito, huko tunakokwenda TANESCO ni lazima iwafuate wateja. Huwa nawaeleza ni mfano kama wa mtu anayenunua daladala kufanya biashara ya kusafirisha watu, halafu anakwenda kumwomba yule mtu atakayetumia daladala nipatie hela niongeze ninunue daladala, maana yake ndiyo hiyo ya TANESCO kuomba nguzo. Kwa hiyo, hiki ni kitu cha mpito ndugu zangu, yatakwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nguzo za ndugu zangu wa Iringa, nimekwenda Iringa nimewatembelea, twendeni na vigezo. Kama mtu ana kiwanda cha nguzo aende TANESCO, ni lazima viwango vya TANESCO tuvikidhi. Hatuwezi kununua nguzo tu kwa kusema kwamba, haya mambo ya ubora hayana uzalendo, kwa sababu mambo yakiharibika mtawageuka tena TANESCO. Kwa hiyo, kama kuna mtu ana uwezo wa kuuza nguzo aje nguzo zake zifanyiwe tathmini na nguzo hizo tutanunua hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, umeme vijijini, REA Awamu ya II hadi sasa hivi ndugu zangu, jana Hazina imeweka bilioni 80.2. Hadi jana Serikali imeshatoa asilimia 80 ya fedha za REA Awamu ya II. Kwa hiyo, huko kwenu mtaona mabadiliko wakandarasi watakavyokwenda kasi, hamna kisingizio na nimemuuliza REA MD anasema hizo akizipata, Wakandarasi wanalipwa na nia yetu ni kazi za REA awamu ya II zote zikamilike ikifika Juni mwaka huu. Awamu ya III, mmeona tumeongeza. Sasa ndugu zangu, tuna shilingi bilioni 534.4 na Hazina kwa kuwa makusanyo yetu yamekuwa mazuri, nina uhakika fedha zote hizo zitapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbali ya hiyo wengine hawakujua kwamba mbali ya hizi fedha, mnazopitisha humu Wizara nayo tunasumbuka, tunazunguka duniani kutafuta fedha. Msidhani ni za bajeti tu! Ndiyo maana Jumatatu msiponiona hapa nitakuwa nimekimbia kwenda kuwatafutia fedha. Mambo yakienda vizuri na tunayejadiliana naye mwingine anataka kumwaga milioni 200 REA, dola sio shilingi! Huko huwa tuna majadiliano kwenye dola tu sio shilingi tena. Kwa hiyo, akimwaga hizo 200 jamani mtakuwa wapi? Sasa tatizo kama hutaki bajeti hii ipite, basi sasa hata hiyo 200 usahau. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, solar kwa watu wa visiwani, nataka kuwahakikishia watu wa visiwani tumeshafanya uamuzi na REA, REA wameshaleta kwangu kwa maandishi kwamba visiwa vyote vilivyoko ndani ya mipaka ya Tanzania vitapata umeme wa jua – solar uzuri wa hii, hii tunaongea tayari tuna pesa, unajua huku Nishati na Madini tunaongea kitu cha uhakika. Tuna hela, wala hatulalamiki ooh! fulani katunyima hela ah ah! Tuna hela! Sasa uzuri wa hizi solar vijijini tunaomba Wabunge mtusaidie vijana waliosoma VETA wanaweza kwenda pale REA waone namna wanavyoweza kuwatumia. Wale vijana wenye utaalam, kuna fedha wanaweza wakapewa pale. Nendeni REA vijana wajikite kwenye huu umeme, tutatoa ajira, tutatoa na fedha na REA huwa inatoa fedha kuwawezesha watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakandarasi nimekaa nao vikao karibu viwili, wale wabovu wote hawatapata miradi tena niseme transformer za TANELEC mimi mwenyewe nilienda pale siyo kwamba waliosema hapa ndiyo wamegundua hilo, ni mimi nilienda pale. Ila wengine tuna kawaida ya kukaa kimya tunafanya vitu kimya kimya, kwa hiyo aliyeongea mambo ya TANELEC hapa siyo yeye wa kwanza, wa kwanza ni mimi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimewaeleza TANESCO na REA kwamba REA Awamu ya III tujitahidi kutumia transformer zetu kwa sababu wenye share kwenye TANELEC ni TANESCO na NDC nao wana share. Hata hivyo, ndugu zangu tatizo ni Sheria yetu ya Manunuzi, kwa hiyo tunaomba Sheria ya Manunuzi iweke sehemu kwamba ni lazima vitu vya ndani vitumike. Kibaya cha Sheria ya Manunuzi hata kama mtu anataka kula rushwa, kudanganya anakimbilia hiyo sheria na nyie ndiyo mliipitisha humu mliokuwemo, mimi sikuwepo hapa wakati huo. Kwa nini mlipitisha hii sheria? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja mafuta, wengi wamelalamika, lakini Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tulisema usimamizi ni mbovu. Sasa hivi TPDC tumeitoa kwenye shughuli ya kufanya biashara, kutafuta mafuta na gesi, wakati huo huo inasimamia makampuni mengine. Kwa hiyo, tumeanzisha PURA (Petroleum Upstream Regulatory Agency). Hii ndiyo itasimamia mikataba yote, kila kitu hata TPDC yenyewe itasimamiwa, itapitia mikataba, itaweka ma-auditor, kwa hiyo, nadhani hapo tutakuwa tumepiga hatua na udhaifu huo utakuwa umetoweka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uagizwaji wa mafuta, vilevile tumeanzisha Petroleum Bulk Procurement Agency, huko nyuma ni waagizaji mafuta walikuwa wamejiweka pamoja wenyewe wanaji-regulate wenyewe, sasa tuna chombo cha Serikali na chenyewe kinafanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa mafuta wengi sana mmeongea EWURA, unajua Waheshimiwa Wabunge kuna mihimili mitatu, unashangaa mtu anayetaka kulazimisha mhimili wake ndiyo uwe na sauti kubwa kuliko mihimili mingine. Mlishatoa pendekezo kwamba EWURA iko Maji, iko Nishati inayumbayumba sasa nyie mmetoa ushauri kwa Executive, kwa hiyo ushauri wenu tunauchukua, tunakwenda kuufanyia kazi, lakini tusije hapa tena unasema tulisema, hapana! Mnashauri nyie, sisi tuna shauri Bunge, sasa ushauri unaweza ukachukuliwa au ukakataliwa. Hiyo ni muhimu sana, ushauri unaweza ukakubaliwa au ukakataliwa! Kwa hiyo, tutalichukua hili kama Serikali tutalifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la vinasaba limekuwa kubwa, mmeliongelea kwa hisia, hatuwezi kuamua hapa. Naitisha na nimeongea na wengine Jumanne kwa sababu nitakuwa nimepewa kazi zingine na wakubwa zangu, lakini Jumanne tarehe 24 yaani Jumanne ya wiki ijayo, saa nne asubuhi nataka nianze kikao cha kutatua hili tatizo la EWURA na vinasaba. Hatuwezi kulitolea uamuzi hapa, tukitoa hapa litakuwa la kisiasa maana sisi wote hapa wanasiasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeita wale wanaohifadhi mafuta, naomba watoe wawakilishi wanne wanaohifadhi mafuta, wawakilishi wanne wanaosafirisha mafuta, wawakilishi wanne wanaofanya biashara ya mafuta, waje pale Wizarani na mimi mwenyewe ndiyo nitakuwa Mwenyekiti, saa nne asubuhi Jumanne tarehe 24, tuyaongee yote waziwazi na EWURA ikae pale ijibu mapigo. Baada ya hapo ndiyo tutaona tunakwendaje, lakini suala la vinasaba hatuwezi kulifanyia uamuzi hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, gesi asilia, LNG fidia italipwa, mmeomba tusomeshe vijana, ndugu zangu fuateni mambo tuliyoyafanya tumesomesha vijana wa Lindi na Mtwara wengi sana VETA. Tumewalipia kuja mpaka hapa chuo chetu. Wakati tunaenda mimi mwenyewe nimeomba scholarships China, wamenipatia scholar 25 kila mwaka kwa miaka mitano. Tunatafuta watu wa Lindi na Mtwara, kwa hiyo watu wa Lindi na Mtwara kusema tuwasomeshe tunajitahidi, ndugu yangu hawa wengine wa China wameshachaguliwa. Kwa hiyo, kama mna vijana muwalete halafu hii LNG biashara yake sio tu ya oil and gas unataka watu ma-chemist wazuri, ma-physicist na wengineo. Kwa hiyo, bado hao tunaotaka kuwasomesha lazima wapambane na mambo ya sayansi. Unajua mambo ya sayansi tena hayana mambo ya mkoa. (Makofi/Vicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge sawa mmesema tutawaita, tutakaa chini, tutaongea na watu wengi wa Lindi na Mtwara, tunaongea sana labda tu hii semina niwaite tena tukae chini, ni bahati mbaya wenzenu tuliwapeleka mpaka Norway, tumewapeleka Malaysia, tumejitahidi sana. Sasa mngewabakiza wale unajua! Haya! Gesi asilia inatumika viwandani sasa hivi tunavyosema kuna viwanda 37 Dar es Salaam vinatumia gesi na vinataka gesi zaidi. Kwa hiyo, ndugu zangu tusidhani kwamba gesi haijatumika, inatumika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, gesi majumbani, tumefanya majaribio, bomba la kilometa 6.3 kutoka Ubungo mpaka Mikocheni nyumba za TPDC wale ndani ya nyumba wana mabomba mawili; bomba la maji na bomba la gesi. Tanzania ya Mheshimiwa Magufuli anayosema ya viwanda ndiyo hiyo hata nyie Wabunge tutaanza na nyie muwe na mabomba mawili la gesi na la maji. Hawa wa TPDC wananiambia kwamba kwa mwezi wanalipa shilingi 25,000 elfu kutumia gesi kupikia, chini kuliko hata mkaa. Kwa hiyo, huko ndiyo Tanzania mpya inayokuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi na Mtwara mnajua tumeshaanza kufanya feasibility studies na huenda tutazipata hizo fedha. Mimi mwenyewe nazisimamia kuzitafuta tutapata hizo fedha, ndiyo maana mwingine akisoma kwenye bajeti anasema mbona hapa mmeweka kidogo lakini hizi fedha ni nyingi, hapana! Sisi tunategemea fedha nyingi nje siyo hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuna Lindi na Mtwara mtapata. Nyie wenyewe Waheshimiwa kwa kuwa ni Madiwani nyumba mjenge zimekaa kwenye foleni vizuri, mahali ambapo bomba litapita maana bomba kulipitisha kwenye squatters ni problem kweli kweli. Kwa hiyo, huo umeme unakuja Lindi na Mtwara na Dar es Salaam ndiyo tumeombea fedha kusambaza gesi majumbani. Sasa na hii gesi haitaishia hapo, Tanzania ijayo ambayo Mheshimiwa anasema ya viwanda anasema vitu vya uhakika. Sasa hivi hili bomba kubwa linasafirisha kwa siku, 70 million cubic feet of natural gas per day, lakini capacity yake ni 784 million cubic feet of natural gas per day! Hili bomba sasa hivi likianza kufanya kazi likijaa kabisa kufanya kazi na kugundua gesi lazima tupeleke mikoani. Kwa hiyo, hata mikoa itapata hii gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, matumizi mengine, Kiwanda cha Mbolea cha Kilwa chenyewe kimepanga kuzalisha tani 3,800 kwa siku. Uwekezaji wake ni dola za Marekani bilioni moja nukta tisa. Sasa ndugu yangu wa Lindi ukisema tunapataje faida, kuna Kiwanda cha Mbolea kinakuja investment one point nine billion US dollars na bado unasema hujui utafaidikaje, saa zingine ndiyo maana huwa unaniona mzee nakaa kimya, nashindwa tu niseme nini sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, matumizi yale ya gesi siyo mengi kiasi hicho, huyu anahitaji 104 million cubic feet of natural gas per day, kwa miaka 20 anakuwa kama amekuna upele tu, hajatumia gesi yoyote, wala kule msianze kuwa na masikitiko gesi yetu, yaani hazidishi TCF moja, havushi trillioni moja ya gesi kwa miaka 20. Ndiyo maana hata wale wa Mtwara wanaweza vile vile wakaanzisha hicho kiwanda na LNG ndugu yangu ukisema huoni faida ndiyo itakuwa investment kubwa katika historia ya nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende Dangote mmeiongelea sana, Dangote wameshindwana na TPDC bei, yeye anataka dola tano kwa unit TPDC inasema nne lakini wameshakubaliana watajenga pipe atatumia. Makaa ya mawe aliagiza South Africa mara moja tu! Tumemzuia atumie mawe ya Ngaka, gypsum nayo tumemzuia atumie gypsum za hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, bomba la Uganda mmeliongelea tutalifanyia kazi, finally tunafanyia kazi, wiki ijayo tutaonana tena kulijadili tena. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije madini. Nyamongo ndugu yangu Heche tulikaa, ndiyo maana akiongea mimi natulia tu! Tuliweka Tume, tutakwenda pale itakuwa wazi. Sasa hayo yote aliyokuwa anaongea humu sijui yako kwenye ile ripoti, kwa hiyo atulie tu!
Mheshimiwa Naibu Spika, Mererani tanzanite, tunajua kuna matatizo ya kufa na kupona lakini tunalifanyia kazi vile vile. Lakini kwa tanzanite, Watanzania sisi wenyewe tuliomo humu huwa tunasema wazawa, wazawa walio na hiyo kitu ni wazawa! Ndiyo maana siku nyingine nilisema, jamani hata mzawa, mgeni wote wanaweza kuwa sio wazuri. Sasa sijui mzawa akikuibia dola kumi na Mhindi akikuibia dola kumi yupi amekuibia nyingi? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, haya kodi, katika mikataba na kodi za madini, ni kweli kwamba kuna migodi ambayo haijaanza kulipa kodi ya mapato (Corporate Tax), lakini karibu yote sasa tunaisimamia wataanza kulipa.
Vile vile Waheshimiwa mmetoa wazo la TMAA, TANSORT na TRA na hilo tunalichukua twende kulifanyia kazi. Wachimbaji wadogo, tumewapatia mlezi wao ni STAMICO, maeneo tunatoa na tutaendelea kutoa. Jumapili iliyopita nilikuwa nimekaa na watu wa World Bank watatoa karibu dola milioni 400 kuwasaidia. Kwa hiyo tunaendelea kuwasaidia sana, isipokuwa na nyie muwahimize walipe kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimalizie na hili la Mheshimiwa Zitto, alisema jamani mafuta mbaani ya siku tano ndege hazitui hapa. Nimepewa hapa takwimu inaonesha hadi sasa tuna lita milioni 8,749,810, haya yanatutosha mpaka Juni, sasa huyu aliyekwambia yamebaki ya siku tano yeye mwenyewe kaleta barua anasema anayo ya siku ngapi? Anayo ya siku 16. Ndiyo mambo nasema haya mambo magumu kidogo, alimwambia ana tano, huyo huyo kaleta barua nina ya siku 16. Kwa hiyo, tunachokifanya ni kwamba tunachukua tahadhari, tunashukuru sana tutaleta mafuta mengine tuhakikishe kwamba mafuta yapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini huyu aliyesema mafuta yake ni machafu kuna sehemu ya hifadhi ya mafuta yake TBS imekuta ni masafi. Kwa hiyo, kuna mengine ana mchafu, huku ana masafi, niwaeleze hawa wa mafuta hii ni biashara ngumu, ni lazima tunavyoijadili humu tuwe makini sana. Huyu aliyeleta ndiye amempatia PUMA, amempatia OILCOM, amempatia TOTAL, amempatia GAPCO. GAPCO ni safi, TOTAL safi, OILCOM safi, PUMA ndiyo analalamika, lakini sehemu ya shehena yake haina hiyo contamination na TBS wanaendelea kufanya utafiti na kujaribu kutafuta nini kimetokea. Lakini mafuta yapo, tunachukua tahadhari yasije yakaisha kabla, meli nyingine inakuja tarehe 13 Juni, kwa hiyo tunataka kuhakikisha tuna mafuta mengi kabla ya tarehe 13 Juni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani nimemaliza sasa? Bunge lako lilikaa, aah! Sorry! Bado bado. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa hoja, kuna moja hapa limebaki la hawa wa magwangala lakini nilitatua. Jamani haya mabaki kuja kukaa dunia ya karne ya 21 unang‟ang‟ana kabisa mtu apewe mabaki ya mgodi, kusema kweli haiendani, kweli! Inaweza kuwa hamna kitu humu. Ni wananchi na CHADEMA ndiyo mlimtuma...

Aliombwa? Wananchi ndiyo walimwomba. Mnyika sasa kama…
Ooh samahani, lakini unajua Mheshimiwa Mnyika, kijana wangu huwa mara nyingi kabla sijamaliza nampatia swali la kichwa. Je, nimpatie, nisimpe?
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, haya naomba kutoa hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia fursa ya kuanzisha mjadala huu. Nianze kwa kushukuru Wizara kwa kufanya kazi nzuri. Vilevile nimshukuru Rais na timu ya Serikali kwa mipango mizuri waliyotuletea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mpango wa Mwaka Mmoja ni sehemu ya Mpango wa Miaka Mitano. Kwa upande wangu niseme kwamba naunga mkono, miradi yote itatekelezwa na hasa ya Jimbo la Musoma Vijijini, ikiwemo na barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyosema na tunavyopaswa kufanya ni kutoa mapendekezo. Kwa hiyo, nianze kwa kusema hivi; kwenye mambo ya uchumi na maendeleo, ukitaka kupunguza umaskini popote duniani, ni lazima uchumi ukue siyo chini ya asilimia 8. Ndiyo maana Ilani yetu ya CCM wale waandishi walikuwa ni wataalam wazuri, tumecheza na asilimia 6 mpaka 7 kwa muda, tumekwenda mbele, lakini wataalam wanasema usiwe chini ya asilimia 8. Ukitaka kwenda kama China ilivyofanya toka miaka ya themanini mpaka leo hii, ni lazima uchumi wako ukue kwa zaidi ya asilimia 10 na siyo chini ya miaka kumi, ishirini, ndiyo unaweza kuwa nchi yenye kipato kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mchango wangu mimi ni namna gani sisi Tanzania tutafanya tuendelee kuwa nchi ya kipato cha kati. Waheshimiwa Wabunge, kipato cha kati kuna madaraja mule; kuna lower middle income, ndimo sisi tumo. Daraja hili maana yake unakuwa na pato ambalo ni kati ya dola 1,026 mpaka dola 4,035. Ndiyo maana Mpango wa Pili ulikuwa unasema Tanzania twende kwenye GDP per capita ya Dola 3,000, tulitegemea hivyo kama miaka ya nyuma huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tumeingia tukiwa na Dola 1,122 na sasa hivi tuko watu milioni 60. Tukifika mwaka 2025 tutakuwa watu takriban milioni 70. Sasa tuchukue kwamba pato letu kwa mmoja mmoja, GDP per capita iwe ni Dola 1,200. Maana yake tatizo la kubaki kwenye 1,100, uchumi ukitetereka kidogo tu, unaanguka chini, unarudi kuwa kwenye nchi ya kipato cha chini. Ndiyo tatizo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi Waheshimiwa Wabunge, tunapaswa kuishauri Serikali tuzidi kwenda mbele. Kwa hiyo, tukiwa na pato la 1,200 kwa watu milioni 70, tunapaswa kuwa na GDP ya Dola za Kimarekani bilioni 68, sasa hivi tuko 50. Tukisema tunasogea kidogo ili tubaki pale katikati, twende kwenye GDP per capita ya 1,500, ukizidisha kwa 70 tunapaswa Serikali yetu na sisi wote tuwe na GDP ambayo iko kwenye Dola za Marekani bilioni 105. Angalia hiyo safari, kutoka GDP ya Dola bilioni 50 kwenda 84, kwenda 104, siyo kazi nyepesi, lakini tunaweza kwenda huko. Kwa hiyo, mapendekezo yangu ni tuone tufanyaje ili tuwe na uchumi unaokua kwa zaidi ya 8%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine cha kuweka maanani ni kwamba daima; na nashukuru ripoti imeweka maanani kwamba sisi ni sehemu ya hii dunia na kwamba tutauza bidhaa zetu kwenye Soko la Dunia. Hiyo ni muhimu sana. Kwenye mambo kama haya ni lazima ujilinganishe na mwenzako. Nami nimechukua nchi mbili tu za kujilinganisha nazo. Nimechukua ya kwanza Kenya ambao ni jirani zetu. Wenyewe GDP per capita yao sasa hivi ni Dola 2,075. Kwa hiyo hata wao wakiyumba hawawezi kushuka mpaka Dola 1,025. Mwaka 2025 GDP ya Kenya itakuwa Dola 2,593. Lazima tushindane nao, wao wamefanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine niliouchukua ni Seychelles. Nimechukua Seychelles kwa sababu wanaojua historia ya nchi yetu miaka ya 1980, bila Serikali yetu au wanajeshi wetu kwenda Seychelles, hali ilikuwa mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, GDP ya Seychelles, kwa kifupi, ndiyo ya kwanza kwa Bara zima la Afrika, lakini tuliwasaidia, tuliwapigania, wametuzidi. GDP per capita yao sasa hivi ni Dola 12,233. Mwaka 2025 GDP per capita yao itakuwa Dola 18,812. Ni kwamba Seychelles itakuwa ni nchi tajiri, itakuwa kwenye higher income. Higher income ni lazima uvuke GDP per capita iende zaidi ya Dola 18,000.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Profesa Muhogo, wale hatuwawezi kwa sababu population yao hata 300,000 hawafiki.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, GDP per capita ni suala la hesabu. Ni kama machungwa, ni hesabu, ni ratio. Ni Gross National Income divided by the population. Kwa hiyo, lazima ulinganishe tu. Hiyo ni hesabu, ni ratio. Ratio ni ratio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hivi, tutafikaje huko na tutabakije huko? Pendekezo langu la kwanza, kama mpango unavyosema, uzito wote tuweke kwenye kilimo. Kwa sababu, kwanza tuna tatizo la ajira, ambalo tutalijibu kupitia kwenye kilimo. Pili, tunahitaji malighafi kwa viwanda vya ndani na vya nje, tutapata kwenye kilimo. Sasa hapo kwenye kilimo tunaendaje? Cha kwanza kabisa, nilimsikia Mheshimiwa Naibu Waziri, alijibu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge na Serikali, mahali pa kuanzia pa kwanza ni suala la mbegu. Hili suala la mbegu ni suala ambalo duniani sasa hivi biashara yake ni bilioni 45 dunia nzima. India inajitahidi katika hizo bilioni 45 inachukua mbili. Kwa hiyo, sisi mahitaji ya mbegu lazima tuyatatue na tutayatatua kwa kuzalisha mbegu zetu na tutayatatua kwa kuwekeza kwenye utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi, walioko kwenye sayansi na mambo ya uchumi ya dunia, tumeona uhusiano mzuri uliopo kati ya ukuaji wa uchumi na utafiti unaofanyika ndani ya nchi hiyo. Haiwezekani, haijawahi kutokea, labda iwe kwa miujiza na miujiza huwa ipo kwamba wewe huwekezi kwenye utafiti, ukaja kuitawala hii dunia, haiwezekani! China na Marekani wanapambana kwa ajili ya utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo, hilo ndiyo pendekezo langu la kwanza kwa upande wa kilimo.

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Bado nadhani.

MBUNGE FULANI: Bado sana, endelea. MWENYEKITI: Bado dakika tano za mwisho. MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Ooh!
Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hizo, nimechukua mazao ambayo lazima tuwekeze sana, kwa sababu yanaliwa sana duniani. Tunaweza tukalima kila kitu, lakini tulime mchele ambao zaidi ya asilimia 50 ya watu wote duniani ambao sasa hivi tupo bilioni 7.8 wanatumia mchele kama chakula kikuu (staple food). Cha pili ni ngano, nayo ni zaidi ya asilimia 50; cha tatu ni mahindi. Mahindi ni chakula na kwenye viwanda. Cha nne, nimechagua muhogo kwa sababu una matumizi zaidi ya 100 na unatumika sana viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa pendekezo langu kwa sekta ya kilimo, tuzalishe mazao ambayo wananchi wengi duniani wanayatumia ambayo ni mchele, ngano, mahindi na mihogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha kilimo, kwa ajili ya muda, ninachopendekeza ni nishati. Naenda kwenye fedha nyingi, siyo ndogo ndogo. Nishati ni lazima tuzalishe umeme kutoka vyanzo vingi. Vyanzo vyetu sasa hivi ni maji na makaa ya mawe. Tumejenga transmission lines za 400KV za kupitisha umeme kwenda Kenya mpaka Ethiopia, kwenda Zambia mpaka soko la SADC huko. Zile lines zinaweza kupitisha Megawati 2,000 kwa mpigo, kwenda au kurudi. Kwa hiyo, eneo lingine ambalo litatupatia fedha nyingi…

(Hapa Mhe. Hussein M. Bashe alikatiza katikati ya Mwenyekiti na mchangiaji kinyume na Kanuni za Bunge)

SPIKA: Mheshimiwa Bashe, rudi ulikotoka, umemkatiza Profesa. Endelea Profesa.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, umeme huu tuutoe kwenye maji, tuutoe kwenye gesi na kwenye makaa ya mawe (coal), halafu na renewable (solar, wind, geothermal na kadhalika).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye coal hatuna hata megawatt moja. tulianza mjadala, tukaiambia dunia kwamba sisi hatujachafua mazingira kwa sababu siyo tu per capita, pollution yetu kwa kila mtu ni 0.22 tones per person per annum, huwezi kulinganisha na China na Marekani ambayo ina zaidi ya tani 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, eneo la pili la kutupatia fedha nyingi ni umeme uwe mwingi, bei itashuka nchini, viwanda vitazalisha kwa bei ya chini na vile vile tunataka tuuze umeme nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo naligusia ni LNG (Liquefied Natural Gas). Tuna gesi kule baharini karibu 57TCF. Ni lazima tuharakishe ili tuweze kupata hizo 15 metric tones per annum ambazo tumepanga kuzalisha pale Lindi. Sasa hii LNG itatusaidia sana kuleta fedha nyingi ndani ya nchi. Ukichukua nchi kama Qatar, nimechukua mfano. Qatar haina uchumi mkubwa wa kutegemea mazao, inategemea gesi tu. Yenyewe GDP per capita ya Qatar ni dola 52,000. Ni among the top ten in the world, GDP per capita ya Qatar na wana-depend on gas. Kwa nini sisi gesi yetu isiharakishe huu uchumi na hizi fedha za mipango yetu tunayoifanya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipanga kuzalisha ule wa kuzalisha, yaani two trains, maeneo ya kuzalisha. Qatar wana 14 trains, hatuwezi kushindana nao. Wenzetu Msumbiji sasa hivi wamejipanga watazalisha train moja 13 million metric tones per annum halafu na nyingine itaenda mpaka 43. Tatizo la Msumbiji wakitutangulia ni kwamba wataweka mikataba ya muda mrefu na nchi ambazo sisi tunataka kwenda kuuza gesi. Kwa hiyo, lazima tushindane na Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nimelileta, nadhani nina muda wangu; nimechukua kwenye fedha nyingi tu. Nilimsikia yule Mheshimiwa Mbunge wa Rukwa akiongea kuhusu gesi ya helium. Sasa hivi duniani, ilikuwa inazalishwa kwa wingi Marekani, kule Texas na Oklahoma, wakaingia nao vita ya kwanza, ya pili inaanza kupungua. Duniani mahitaji ya helium ni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Profesa.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Kwa hiyo,…

MWENYEKITI: Nakushukuru sana.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema kwamba hii gesi ambayo tunayo nyingi sana, kwa makisio ya awali ya wale vijana wa Oxford ni kwamba tuna 2.8 billion cubic feet; na sasa hivi Soko la Dunia ni six billion. Kwa hiyo, tunaweza ku-sustain Soko la Dunia kwa miaka kati ya 20 mpaka 30, hatutakuwa na tatizo la kung’ang’ana na uzalishaji mdogo mdogo wa viazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwamba, Mheshimiwa Shangazi ambaye atakuwa wa pili baada ya mimi amenipatia dakika tano zake kwa sababu, anadhani naweza kuwapa mambo mengi mazuri. Halafu… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Profesa sasa changamoto ni kwamba, kipindi hiki unachangia tu dakika kumi. Kwa hiyo, zile za kwake inabidi labda umgawie mtu ambaye hayupo kabisa na achangie hizo tano peke yake kwa hiyo, muda wako utaanza sasahivi wa hizo dakika kumi.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, haya. Ombi lingine ni kwamba, dakika kumi nikijadili tu la Liganga/Mchuchuma hazinitoshi kwa hiyo, kama Bunge mnataka kusikiliza ya Liganga/Mchuchuma mniombee dakika tano badaye. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Waheshimiwa Wabunge naomba nichangie na kutoa ushauri huu. Ni kwamba, mpango tulionao makusudio makubwa kwanza ni suala la ukuaji wa uchumi uende zaidi ya asilimia 8, mbili ajira, tatu ustawi wa jamii na maendeleo, yote yameelezwa humo, ila mimi ninaboresha na kuongezea.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huu unahitaji kuhudumia watu, sasa hivi tuko watu karibu milioni 61 mwaka 2025 tutakuwa takribani watu milioni 70 kwa hiyo, huu mpango lazima uwahudumie hawa watu. GDP per capita yetu iliyotuingiza kwenye nchi za kipato cha chini (lower middle income) ni dola 1080. Maoteo ni kwamba, tukifika mwaka 2025 GDP per capita yetu itakuwa ni dola 1400. Hizo bado ni fedha kidogo ndugu zangu, inamaanisha mwaka 2025 kipato cha Mtanzania kila mwezi kitakuwa dola 117.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikaja na hesabu angalao tufike dola 150 maana yake kwamba, GDP per capita yetu itakuwa dola 1800 tukifika mwaka 2025 ambayo wenzetu wa Kenya tayari wanayo. Sasa kinachohitajika hapa na ugomvi mwingi wa kodi, task force, nionavyo ni kwamba, hata kodi zetu tufanyeje tatizo bidhaa ni hizohizo na walipa kodi ni haohao. Na huu uchumi tukitaka ukue kwa zaidi ya asilimia 8 ni lazima tutafute bidhaa mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye bidhaa mpya naomba mnisikilize kwa makini. Tumefanya utafiti kutoka miaka mingi karibu miongo mitatu, tumeangalia nchi zilizokuwa na mafanikio makubwa ambazo uchumi ulikuwa kwa zaidi ya asilimia 10 kwa mwaka tumegundua kwamba, uwekezaji wao mkubwa namba moja ulikuwa kwenye utafiti. Ninaomba huu mpango tulionao uweke mkazo kwenye utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Jirani yangu hapa alivyosema tumeshakubaliana nchi za kiafrika 1% of the GDP iende kwenye research and development. Kwa hiyo, mpango huu tunaomba utoe fedha nyingi kwa ajili ya utafiti, lakini kwa hali ya sasa tuliyonayo, COSTECH tuliyonayo haiwezi kufanya hiyo kazi kwasababu muundo wake ni kama idara ndani ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanya kazi na ma- funding agencies mengi sana duniani, lakjini hayana muundo kama wa COSTECH. Bajeti ya COSTECH ni ndogo, ukichukua 1% ya 50 billion US Dollars ya mwaka, sasa hivi nadhani GDP yetu karibu iko kwenye around 60 billion uchukue 1% hiyo, mnajua hesabu, uipatie COSTECH, COSTECH haiwezi ku- manage hizo fedha kwa ajili ya muundo na haiwezi kufanya utafiti. Kwa hiyo, cha kwanza kabisa kwenye mpango wetu turudi kwenye utafiti. Kilimo ni utafiti, maji ni utafiti, ujenzi ni utafiti, hatuwei kulikwepa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije kwenye bidhaa mpya ambazo zitaleta 8% au 10%. Cha kwanza kabisa nadhani msemaji mmoja jana alisema kwenye sekta ya madini lazima tubadilike ndio maana nilisema ya Liganga siwezi kuongelea mambo ya iron. Dunia inabadilika kuna madini yanatakiwa sasa hivi duniani kwa hiyo, kwenye ripoti zetu kuwa tunaongelea kila siku dhahabu, tanzanite, ni kama tunapitwa na wakati kidogo lazima tulete madini mapya ambayo ndio yatafanya uchumi ukue kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, na haya madini mapya yanahitajika kwenye fourth industrial revolution, mabadiliko, hata kama sisi hatuhusiki tutachukuliwa tu kama ma- passenger, passive passengers in the fourth industrial revolution ndio sisi, lakini tunayo hayo madini. Kwa hiyo, mpango wetu badala ya uongelee vizuri dhahabu, ongelea tanzanite, lakini hiyo ni monotony, madini yanayohitajika sasa hivi naomba niyasome; lithium kwa ajili ya mabetri, cobalt, nickel, platinum, chrome, manganese, copper. Hayo yote nchini yapo, lakini hatuna mgodi hata mmoja, badala ya kila siku kufukuzana na dhahabu tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na niwasaidie tena. Dhahabu sasahivi imepanda bei kutoka kwenye dola 1700 mpaka dola 2000 kwa ounce, lakini nyuma ilikuwa chini yad ola 1400. Kwa hiyo, hesabu zetu mtu akisema sekta inafanya vizuri anasahau kwamba, bei kule imepanda ndio maana tumepata fedha nyingi, lakini haijamaanisha sekta inafanya vizuri migodi ni ileile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna madini ambayo ni muhimu sana. Wote wenye iphone hapa, kama kuna mtu ana iphone, madini yaliyomo humo rea earth elements ni manane, specific eight. Madini haya yako 17 na haya ndio madini yanahitajika sasa hivi duniani zaidi kuliko chuma kwa hiyo, tuwekeze huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado dakika tano?

Mheshimiwa Naibu Spika, bidhaa nyingine ambayo inabidi kutuletea hizo fedha ni nishati. Nishati tutumie nyumbani, nishati tuiuze. Tumeshajenga transmission lines kwenda Kenya, transmission lines kwenda Zambia yaani kwenye soko la SADC na kwenye soko la East African community kwa hiyo, umeme tulionao ni mdogo. Kila siku nasikia mnaimba hydro, ukweli ni kwamba, anayejua mambo ya umeme hydro kukupatia faida umewekeza hela nyingi unahitaji miaka u-re-crop ile faida ndio umeme uwe wa bei ya chini wa maji. Sio tu kwamba, leo nikimaliza bwawa hapohapo bei ni ndogo, labda kama hutaki kurudisha fedha zako.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndugu zangu tulitengeneza energy mix. Na projections ni kwamba, Bara la Afrika litakuwa na ukame tutakuwa tunapoteza kati ya GDP 1% to 2% zitapotea. Je, mabwawa yetu yakikumbwa na ukame nini kitatokea?

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana tunataka energy mix, hydro, natural gas, coal. Tunaenda renewables, wind, solar, geothermal, biomass, tides and waves. Umeme huu tunahitaji na tulishapanga zaidi ya megawatts 10,000 ndio target. Kwa hiyo, huu mpango lazima ujielekeze kuzalisha zaidi ya megawatt elfu kumi kwa miaka mitano ijayo; hii mingine yote haitoshi, tuzalishe tuuze, bidhaa hiyo nyingine mpya hiyo. Na tukipata bidhaa hizi tukauza tukapata fedha nyingi hata tutapunguza hizi kodi tunazopigana kila siku kwa sababu ni bidhaa zilezile ni watu walewale, sasa tulete bidhaa mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuzalishe tuuze bidhaa bidhaa hiyo nyingine mpya hiyo, na tukipata bidhaa hizi tukauza tukapata fedha nyingi hata tutapunguza hizi kodi tunazopigana kila siku kwasababu ni bidhaa zile zile ni watu wale wale sasa tulete bidhaa mpya. Bidhaa mpya nyingine ni ya gesi tumesimama LNG yetu uwekezaji ndio ungelikuwa mkubwa kwa historia ya nchi hii, ni thirty billion, sisi ni thirty billion. Msumbiji vita yao huku Cabo Delgado ikitulia uwekezaji wao unatuzidi, wao wako kwenye sixty billion tumechelewa kwasababu hatujafanya maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo LNG ndugu zangu, natural gas ni bidhaa mpya ambayo nchi kama Qatar ina GDP per capital ya zaidi ya sixty thousand USD per person per annum, na sisi tulipokuwa tumepanga kufika Dola elfu 3,000 per Person per annum tutafikia kwa kutumia uchumi wa gesi. Kwa hiyo huo mpango kama tunataka kufanikiwa mimi sioni kwanini tusirudi kwenye mipango yetu ya uchumi wa gesi, bila hivyo ndugu zangu hatuwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine bidhaa mpya nimekuja nayo ambayo tunabidi kuifanyia kazi ni gesi ya helium ambayo inatakiwa duniani. Wote huwa mnaenda kwenye MRI Scanner. Unajua scanners zote za dunia nzima zinatumia helium, simu zote tulizonazo kuna helium. Kwa hiyo nimechukua bidhaa ambazo zinatumika duniani kwa watu wengi ndio bidhaa mpya. Kwa hiyo ndugu zangu na hiyo nayo tuiendeleze.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ya mwisho hii niliongea wakati ule kwamba agriculture yetu ichukue mazao manne ambayo yanatumiwa zaidi ya nusu ya wakazi wa dunia hii. Sasa hivi tupo watu bilioni 7.8, tukifika mwaka 2025 tutakuwa takriban kwenye bilion tisa. Hawa watu wote hayo madini niliyokwambia wana simu, wana laptop, wanaenda kwenye electric cars na kwa hiyo watatumia hivyo vitu; ndiyo bidhaa mpya ya kufanya uchumi wetu ukue.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mwisho ni kilimo kwa kuwa kinaajiri wengi. tulime na tufuate ile Maputo Declaration. Mwaka 2006 nchi za Kiafrika zilipokuwa Maputo zilikubaliana kwamba angalau asilimia 10 ya pato la Serikali iende kwenye bajeti za kilimo, lakini sisi bado tuko kwenye asilimia tatu hadi nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kilimo, hiyo irrigation mliyokuwa mnaongea jana itafanyiwa kazi, utafiti utafanyiwa kazi, tuzalishe haya manne; yaani Mahindi, Mpunga, Ngano na Mihogo, hayo ndiyo mazao ambayo zaidi ya 50 percent of the world population wanafanya consumption.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hili la Liganga; muda umekwisha au bado upo?

MBUNGE FULANI: Bado.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Haya, kumbe nimeenda kasi, kumbe nimeenda vizuri. Sasa ndugu zangu Liganga ni hivi …!!!

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Profesa naambiwa kengele ya pili imegonga.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, bado wanataka ya Liganga kidogo Mama Mheshimiwa.

NAIBU SPIKA: Dakika mbili malizia.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, haya dakika mbili, jamani ya Liganga Historia yake ni kwamba utafiti ulianza tangu miaka ya 70. Miaka ya 80 Profesa Marehemu Nicas Mahinda alifanya Ph.D yake kuhusu Liganga. Wakati wa miaka ya 80 watu kwenye hiyo Liganga walikuwa wanataka chuma peke yake, lakini ndani yake kuna titanium na vanadium. Kwa hiyo discussion ilikuwa tutatoaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana huu mradi nadhani sijui kama tulifanya vizuri kumpatia mtu mmoja miradi yote miwili; sidhani. Lakini wakati ule mawazo ilikuwa lazima tumpe anahitaji umeme mwingi ili atenganishe Iron kutoka kwenye Titanium na vanadium, zile zilionekana ni madini yasiyotakiwa wakati ule; lakini tekinolojia ya sasa tunayahitaji mno, titanium na vanadium tunayahitaji sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi pendekezo langu kwenye huu mradi, huyu tumempatia vyote, na Makaa na Mawe ya Mchukuma yalikuwa yazalishe six hundred megawatts, megawatts 250 azitumie kwenye mambo ya plant yake megawatt 350 apeleke kwenye national grid. Sasa sijui, kosa tulilolifanya yeye kama huku haweze kuzalisha umeme inamaanisha hata huku kwenye chuma hata zalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nilikuwa nashauri, NDC haina uwezo wa kuendesha huu mradi kwasababu imekaa nao tangu miaka ya 80, lazima tufanya maamuzi huu mradi upelekwe kwa watu wenye ujuzi, wanaoyajua hayo madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile NDC wamepewa soda ash kule Engaluka, hawawezi na wenyewe watolewe hii miradi hao NDC ipelekwe chini ya Ofisi ya Rais kwamba kila Waziri pale anaitwa au Ofisi ya Waziri Mkuu, lakini NDC ikibaki viwanda na Biashara kama imeshindwa kuendeleza huu mradi kwa miaka zaidi ya 40 sidhani kwamba wana uwezo huo, na hawana uwezo huo ukweli ndio huo. Sasa ambacho mimi nilikuwa nimemuomba yule mwekezaji ni wa kutoka China; na mimi napokea ripoti zote za mambo ya madini takriban ya dunia nzima. Nikampendekezea kwamba wewe mimi nadhani mtaji wako na teknolojia yako inaweza ikakufanya huu mradi usiutekeleze. Nnikamuomba balozi wa wakati huu tukakaa, mimi na balozi na yule. Nikasema kwakuwa huyu ameshawekeza hela zake sisi tutafute kampuni nyingine kubwa ya China ishirikiane nae,

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ndugu zangu China ni miongoni mwa wazalishaji wa chuma wakubwa na watumiaji wa chuma wakubwa yaani na wao wataenda kwa speed yao. Kwa mfano mpaka Ijumaa iliyopita walikuwa na tani zaidi ya milioni 100 kwenye bandari zao 43; wanaita stock pile, sasa kama mtu ana stock pile ya tani zaidi ya 110 kwenye Bandari 45 za China je, atakuwa na moto wa kuja kuchimba chuma yetu? (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe na mimi rambirambi za kutoka Musoma Vijijini kwa maafa na majonzi yaliyotupata, tunaomba wapumzike kwa amani. Vile vile katika mjadala wetu tunaoufanya sasa, nadhani tutakuwa tumejifunza na bajeti tunayoitayarisha, mambo yaliyotokea MV Bukoba na yaliyotokea juzi tutayaona kwenye mipango na bajeti ya mwaka ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mjadala wetu ni lazima kwanza tujue malengo yetu. Mipango tunayoifanya iko ndani ya mipango ya miaka mitano ambayo inaisha 2025, ambayo malengo yake ni ukuaji wa uchumi, upatikanaji wa ajira mpya na huduma bora kwa wananchi. Ndiyo maana kwa vyote hivi hatuwezi kukwepa pendekezo ambalo tumerudia mara kwa mara kulitoa, kwamba lazima tuwe na Planning Commission ambayo iko ndani ya Ofisi ya Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa malengo yetu ambayo yako kwenye hiyo document inasema kwamba, ikifika mwaka 2025 tunataka GDP per capita yetu iwe dola 3000. Hiyo inamaanisha kwamba ikiwa sasahivi tuko watu takribani milioni 62, kufika 2025 huenda tutakuwa milioni 68 lakini tunaweza tukafika milioni 70. Maana yake ni kwamba ukichukua GDP per capita ya dola 3000 kwa kila mtu kwa mwaka, tukifika 2025, tunapaswa kuwa na GDP isiyopungua bilioni 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi GDP yetu ni dola bilioni 62. Kwa hiyo huu mpango na bajeti yake ni lazima ituweke kwenye barabara ya kutoka bilioni 62 sasa kwenda kwenye bilioni 200; ni kazi kubwa kweli kweli. Na hapa lazima mipango yetu tuelezane ukweli, tuone kama hilo lengo la GDP per capita ya dola 3000 lilikuwa sahihi au tuliandika tu kwa haraka haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi sisi tukiwa na bilioni 62, GDP per capita yetu inakadiriwa mwishoni mwa mwaka kuwa dola 990. Kwa maneno mengine tumerudi chini, na hivyo tutaenda kwenye group la nchi masikini kufuatana na viwango vilivyowekwa na Benki ya Dunia tarehe moja Julai mwaka jana. Kwa hiyo tumeshuka, tusiongelee uchumi wa kati, hatuko huko tena, tumeshuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huohuo sisi tukiwa hivyo, wenzetu wa Kenya ikifika mwisho wa mwaka huu sisi tukiwa na GDP ya dola bilioni 62, wao watakuwa na GDP ya dola bilioni 107. GDP per capita ya Kenya, mwisho wa mwaka huu itakuwa ni dola 1,550, sisi tutakuwa ni dola 990. Kwa hiyo ukichukua yale ma-group yaliyotengenezwa na World Bank, Jirani yetu Kenya ambaye tunataka kumpatia na gesi yetu, yeye yuko kwenye Lower Middle-Income Country ambayo inaanzia dola 1046 mpaka dola 4095. Sisi tuko chini tuko dola 990, Kenya wapo dola 1,550. Kwa hiyo haya tunayoanza kuyajadili leo, mapendekezo yangu ni haya: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo yetu ni lazima tupunguze mfumuko wa bei (low inflation), mipango na bajeti yetu. Inflation August mwaka huu ilikuwa 4.6%, Septemba imepanda imekuwa 4.8%. Hii lazima tuipunguze, ndiyo tuyajadili, tushawishi Wizara ipunguze. Lengo la pili muhimu kwenye mambo tunayoyapanga na bajeti yake na inafanyika duniani kote, wanapunguza low inflation halafu wanapunguza na interest rates. Ikiwa inflation itapanda inamaanisha benki nazo zitapandisha riba zao za mikopo. Kwa hiyo huu mpango na bajeti yake lazima tulenge huko kwamba interest rates zisipande, zikipanda hata waliokopa nyumba, baiskeli na magari lazima zipande.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho tunapaswa kukiongelea kwenye hii bajeti ni kuzuia Government Bonds (hatifungani) kutumika pasipokuwa na malengo sahihi. Maana yake ukiitumia, inflation ikiongezeka, utalazimika kutumia hii hatifungani. Ukishaitumia ujue sasa umeleta matatizo kwa uchumi wa nchi. Kwa hiyo hili nalo, hii bajeti ije itueleze namna ya kuzuia kukimbia kutumia Government Bonds, kututoa kwenye matatizo ambayo tungeweza kuyatatua kwa njia nyingine kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile mipango tunayoijadili na uchumi wake, lazima ituelekeze ambapo wachumi wanatueleza. Unajua kuna wachumi wa aina mbili na inabidi uchague unapenda kumsikiliza nani. Kuna wale waliochukua econometrics kama akina marehemu Prof. Rweyemamu na kitabu chake cha miaka ya 1970; halafu kuna wale ambao ni political economist, hao maneno ni mengi na hesabu zao za kujumlisha na kutoa tu. Sasa inabidi sijui unataka kumsikiliza yupi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ukichukua wataalamu wa uchumi kabisa wanasema duniani ukitaka kupunguza uchumi ni lazima uchumi wako ukue kwa zaidi ya 8%. Kwa hiyo hii mipango lazima itueleze, kwa sababu mwaka 2020 uchumi ulikua kwa 2%, mwaka jana kwa 4.5% na mwaka huu tunategemea kwenda kati ya 4% na 5%; na mimi takwimu zangu nazitoa kwenye vyanzo ambavyo dunia inaviamini. Unaweza kuwa na chanzo chako kama huko duniani hawakijui, sipendi kukitumia hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa China, ukisikia China kufanikiwa kiuchumi, kwa zaidi ya miaka 20 uchumi wao ulikuwa kwa kadiri ya asilimia 15 mpaka asilimia 20; kwa miaka 20 ndipo China ikafika hapo ilipo. Sasa sisi tunataka tu tufike 8% growth. Kwa hiyo mapendekezo yangu ni kama haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji ili uende kasi, ndugu zangu lazima tuwe na bidhaa nyingi na mpya kwenye soko, siyo kuongeza tozo. Tozo na kodi hazikuzi uchumi. Kinachokuza uchumi ni bidhaa kwenda kwenye soko la ndani na soko la nje. Kwa hiyo hii bajeti, mipango yetu na bajeti, tueleze hivyo, halafu lazima itueleze ajira mpya. Hili neno mpya, siyo zilezile. Ajira mpya ni zipi na kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, itueleze mzunguko mkubwa na mpana wa fedha kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, tufanye yafuatayo: mimi nina mapendekezo yangu kwa wataalamu kwamba twende kwenye kilimo, kwani kina asilimia 30 ya GDP yetu. Hebu tupigane tufikishe asilimia 40. Sasa sitaki kurudia, haya nilishayaongea. Mazao ambayo ni lazima tuyawekee mkazo ni yale ambayo tunatumia ndani ya nchi na nje ya nchi yana soko, ambayo ni mahindi, mchele, ngano, mihogo, matunda na mbogamboga. Haya yote matumizi yake duniani kila siku ni kati ya asilimia 40 na 60 ya watu waishio duniani, twende huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, uvuvi na ufugaji. Samaki watoke ziwani, watoke baharini, tuongeze nyama na maziwa. Hapa uvuvi na ufugaji tukazane tuchangie angalau 5% ya GDP yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, madini. Tuendelee na Tanzanite, Gold na Diamond. Pia kama nilivyowahi kuwaeleza hapa, kuna madini ambayo ni muhimu na yana thamani kubwa kuliko haya. Haya ni lazima mipango na bajeti hii itueleze inavyoiwezesha geological survey. Haya madini yatapatikana kwa kutumia geological survey, siyo Tume ya Madini. Tume ya Madini inasimamia, sasa utasimamiaje huna kitu kipya? Tuwapatie geological survey waendelee kufanya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna madini ya electronics industry, yanayotumika kwenye electronics kama Palladium, Lithium, Copper, Tin, Nickel, Gold na Aluminum. Computer zozote tulizonazo zina Lithium, Cerium, Europium, Samarium, Neodymium na madini mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ugomvi mkubwa sasa hivi unaendelea wa microchips kati ya Marekani na China kama mnafuatilia. Kwa sababu hizi hata simu zenu zote zina microchips. Computers zote na electronics zote madini yanayotakiwa humo ni Sillicon na rare earth element 17, niliwahi kuyataja humu, sina haja ya kutaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya madini, atakayetusaidia kuyapata ni geological Survey, wawekeze wafanye utafiti, watafute madini mapya yanayohitajika duniani, yanaitwa technology metals. Sasa hapa madini tujipige mpaka tufikishe asilimia 15 ya GDP; wanakaribia 10, lakini uchumi wetu uwasukume twende kwenye 15% of our GDP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho ni muhimu na ukiona katika mapendekezo yangu nimeanza ajira ya watu wengi naenda napungua kilimo, uvuvi, ufugaji, mining na sasa uchumi wa gesi. Yote hayo yalitushinda tukadhani uchumi wa gesi, ndiyo utatutoa, lakini tukaamua kuweka kapuni. Sijui kama tutasalimika tusipotoa huko kapuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba uchumi wa gesi una vitu vitatu muhimu; tutazalisha umeme mwingi wa bei nafuu na ujenzi wa mitambo yake ni wa haraka. Halafu umeme wa gesi hauna jua, hauna ukame, tuta-export LNG tunayotaka kuijenga pale Lindi, ni biashara kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu muhimu kabisa, ni petrochemical industrials. Hapa kabla hatujamuuzia mtu yeyote jirani yetu tunayeshindana naye gesi, lazima tujiulize: Je, tukimpa gesi yetu, atakuja na viwanda haraka atuuzie bidhaa zinazotokana na gesi yetu? Hilo ni suala la muhimu sana. Petrochemical industries mfano wake ni mbolea, plastics zote, viti vyote mnavyokalia, vyote ni gesi; sabuni, detergents nyingine, drugs, madawa ya wadudu, rangi na insulating materials. Viwanda ni vingi sana vya gesi. Kwa hiyo, napendekeza hapa hii gas economy ituchangie kati ya 15 na 20% ya GDP. Huu mpango…

MWENYEKITI: Profesa, hiyo ni kengele yako ya mwisho, nakuongeza dakika tatu.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wewe Mwenyekiti ni mwema bwana. Nyingine ya tano ni tourism. Kufika Aprili mwaka huu 2022, tourism imeingiza dola bilioni 1.5. Sasa jamani, tujitahidi tourism tujitahidi ituletee 12% ya GDP yetu, hapo uchumi utakuwa mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, nimeandika, sports, games, music na culture vitupatie GDP mbili. Mwisho ni climate change. Tunataka kuiona hii bajeti inaongelea hili, maana yake matatizo yamekuwa mengi. Sasa hivi Carbon dioxide emission za Tanzania per Capita; tunavyochafua mazingira kwa kila mtu kwa mwaka. Kwa mwaka 2020 ilikuwa 0.18 metrics tons a person per annum. Mwaka 2019 ilikuwa 0.21 metric tons per person per annum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutengeneze mpango na tuje na bajeti. Ndiyo maana kwa kumalizia ni kwamba haya yote niliyoyataja hatuwezi kuruhusu Wizara moja inayapanga yote, mengine hayapo kwao ndiyo maana tunahitaji Planning Commission. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia fursa hii. Nianze kwa kuunga hoja kwa matumaini kwamba Wizara inaenda kubadilika. Ukweli ni kwamba ukisikiliza fedha, unaelezwa mabilioni kama huna uzoefu na hii sekta utaona ni fedha nyingi sana lakini niwaeleze ukweli ni kwamba Sekta ya Madini haijachangia ipasavyo na sababu ni hizi; Sekta ya Madini ingechangia ipasavyo ukuaji wetu wa uchumi unaopaswa kuondoa umaskini lazima ukue kwa asilimia nane mpaka kumi. Narudia tena ukiwa chini ya hapo hata ukifurahiaje hautautoa umaskini. Umaskini wetu lazima upungue utoke kwenye asilimia ishirini na mpaka kumi na tano na inayoweza kutupeleka huko ni sekta ya madini, gesi na vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mwaka toka 1961, miaka 60 iliyofuata mpaka 2021 ukitaka kukubaliana nayoyasema ni kwamba Sekta ya Madini muda mwingi imejishughulisha na utawala wa Sekta ya Madini (Administration of the Mineral Sector) na ndio maana madini yanayochimbwa ni hayo hayo yaani dhahabu, almasi, na vito hasa Tanzanite na rubi. Ndio maana ya Liganga na Mchuchuma nitayaongea siku nyingine, wasingeshughulika na mambo ya utawala sana Chuma ya Liganga toka miaka ya 60 tungeshachimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uchumi wa dunia ya leo msemaji mmoja ameongea vizuri sana sijui kama walimuelewa Profesa Mkumbo ameongea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa leo wa dunia whether wewe ni m-socialist, m–Marxist kwanza ni vitu vimepitwa na wakati havijadiliwi sasa hivi. Uchumi wa dunia sasa hivi unaoongoza ni wa aina mbili, ni private wealth yaani capitalism ya ubinafsi ambayo ndio nchi za magharibi na uchumi mwingine ambao umekuja kuibuka kwa nguvu sana ni state capitalism, nadhani ndio Profesa Mkumbo alikua anaongelea hiyo. Hii state capitalism inafanywa China imefanikiwa, India imefanikiwa, Brazili imefanikiwa, Norway inafanikiwa. Brazili ile kampuni ya PetrolBras ni ya Serikali, Norway kampuni tunayofanya nayo gesi ni ya Serikali hiyo ndio inaitwa state capitalism. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sekta hii ya madini ni lazima itupeleke huko na ndio maana yule nilimsikiliza kwa makini ni lazima iwepo migodi inayomilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la hivyo hatutatoka tutakuwa tunadhani hizo bilioni ni hela nyingi lakini ni ndogo sana. Sasa kuanzia 2023 na kuendelea ndio maana nimesema naunga mkono nadhani tutakuja na hybrid. Tuchanganye hizi kampuni binafsi lakini za Serikali lazima ziwepo. Sasa ina maanisha kwamba Sekta ya Madini kuanzia sasa ijihusishe na uwekezaji, development na kufanya haya tunahitaji taasisi mbili muhimu sana, ya kwanza ni geological survey. Ni ajabu kwamba Tume ya Madini inapewa umuhimu bado ni makosa yale yale ya kushughulika na mambo ya utawala wa madini badala ya kuwekeza geological survey. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa geological survey ni lazima tuwekeze ndio itatueleza tuna madini ya aina gani, kiasi gani ambayo tunataka kuendelea na utawala wa madini lakini geological survey haijawekezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Wizara ya Madini sio lazima ione kwamba hii ni Wizara ya Elimu. Huko zamani tulivyokuwa chuo kikuu sisi, tulikuwa tunafanya kazi na geological survey kwa sababu ukitaka wataalam wengi wapo UDOM, wako Chuo Kikuu Dar es Salaam. Maabara zile lazima ziwezeshwe, haya madini mapya tunayoyaingia haya ninavyoelewa hatuna maabara zinazoweza kutusaidia hapa nchini. Kwa hiyo, mtaendelea kupokea ripoti kutoka nje ambazo nyie hamuwezi kuthibitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna mapungufu makubwa sana na ndio maana tunaanzisha sheria hata hazijatumika tunakuja tunazibadili. Sheria moja ambayo ina mapungufu sana lakini mtu anaweza kushangilia akaifurahia ni hii mpya inayosema tunapata hisa asilimia 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wanaonisikiliza hili ni kosa kubwa tunalolifanya. Asilimia 16 hiyo tunaweza tusipate kitu kwa sababu moja hivi. Hatuko kwenye bodi inayofanya maamuzi, kwenye menejimenti ya juu haupo, haujui unazalisha kiasi gani, haujui unauza kiasi gani, wewe umekaa pembeni unasubiri tu uletewe fedha eti una hisa asilimia 16. Maana ya kuwa mwanahisa ni kwamba ni lazima ushirikiane na mwenzako kuwekeza, kwenye faida mshirikiane na lazima mshirikiane nae kwenye hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa cha kujifunza Watanzania na naomba hii Wizara iende pale Mwadui, mwingine alitaja Mwadui ichukue ripoti ya Marehemu Ally Nuhu Kassim. Kassim alikuwa anafanya kazi nchi za nje akaomba nafasi amepata cheo kwenye UN lakini mwalimu akamrudisha mwaka 69 akampeleka pale Mwadui. Msomi mzuri wa Uingereza akamwambia hebu tunataka kutaifisha hebu angalia Mwadui inavyokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, alitoa ripoti ambayo kwa kifupi inasema kwamba hawaelewi nini kilikuwa kinaendelea pale Mwadui. Watanzania hawaelewi, kwa hiyo, Mwadui tulianza na shares 50 kwa 50. Tumekwenda De Beers ilivyokuja kuchukua, De Beers ikachukua 50 kwa 50 wakasema wanajenga plant mpya nzuri ya kisasa Tanzania, mwenzetu changia hela, sisi hatuna tutaelewana huko huko. Wewe leta tu plant wakasema sawa wakaleta plant shares zetu zikashuka kutoka 50 zikabaki 25. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijui kama Mwadui kama Tanzania kama bado ina share kama Serikali. Kwa hiyo, hii asilimia 16 ndugu zangu Waheshimiwa nawaambia ni kosa ambalo lazima tulirekebishe kwa sababu hatuna nazo control. Huenda hata tusipate kitu, au tukipata inakuwa kidogo sana. Kingine ambacho tunahitaji umakini mkubwa na Wizara ifanye ni madini mapya na leseni wanazotoa. Nitawatolea mfano hapa, leseni zimeshatolewa za PGM (Platinum Group Metals). Je, tunajua huko wanaenda kuchimba nini? Maana yake PGM hii group ina madini kama saba na yote yana thamani ndio kuna platinum, kuna palladium kuna nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nawapa mfano mmoja hapa kwenye hii group, kuna madini yanaitwa rhodium, wakati dhahabu ilikuwa ni dola 1,850 kwa ounce, rhodium ilikuwa ni dola 10,300 kwa ounce. Je, sisi tunajua hawa tuliowapa leseni watayachimba hayo? Unakuja kwenye rare earth elements wanasema madini ya mkakati, je ni ya mkakati kwako au ni ya mkakati kwa wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii rare earth element kama mtu haielewi anaiongea tu kwa mzaha mzaha ni madini 17, element 17 ziko kwenye hii group na zote zina thamani kubwa ndio hayo Marekani wanaita ya kimkakati, Ujerumani, Japan. Sasa katika haya madini yapo matatu makubwa kabisa, lutetium, lanthanum, scandium. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue moja nieleze, lutetium inatumika kwenye X-Ray hata kwenye treatment ya kansa. Treatment ya kansa ikiwa na haya madini ambayo yanaitwa 177 PSMA, kozi moja ni dola 10,000 na treatment inataka kozi moja mpaka nne. Kwa hiyo, ni between 30 and 40 thousand US Dollars. Ndio maana wanasema haya madini ukitaka kuyanunua unaweza ukaingia kwenye mabilioni ya dola. Je, leseni tunazozitoa za rare earth elements tunajua ni madini gani tumewaambia wachimbe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana badala ya kuwekeza hela nyingi sana kwenye Tume, mimi ningewekeza geological survey na kwenye taasisi zetu za geology. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna madini mengine la mfano ni scandium inatumika kwenye aerospace, kwenye mid fighters hasa za Warusi hata wanaocheza golf wanaitumia hii. Yenyewe kilogram moja ni dola 3,912 na duniani kwa mwaka zinahitajika tani kati ya 15 na 20 tons mwaka mzima. Haya yako kweye rare earth elements. Je, tunajua leseni tunazozitoa? Je, tunajua hiyo 16% tuliyopewa ya bure tunaijua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije topic nyingine ambayo nimeiongelea kwa muda leo naichukua kwa njia nyingine na ninashukuru Wabunge nao wameongelea suala la kuwa na reserve ya dhahabu (gold reserve). Niliongea leo sitarudia ila nachukua angle nyingine ya kuwapa taarifa wale ambao bado wanasita sita kwamba kwa nini unahitaji kuwa na gold reserve? Kwa hiyo, nimeenda kwa wale wanaotukopesha, nimeenda kwenye World Bank nikaangalia hisa za World Bank ambazo zinaendana na voting powers. Yaani unavyozidi kuwa na hisa nyingi ndivyo ambavyo kura yako inazidi kuwa nzito. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo World Bank nimechukua tatu. Marekani voting powers za Marekani ni around 17%. Japan ni around 8.55%. China ni 2.25%. Sasa angalia Marekani mwenye voting power kubwa kwenye World Bank ana dhahabu reserve tani 8,133 tons gold reserve. Huyu Japan anayo vote kwenye hii IDA (International Development Association) World Bank ina mikopo ya aina mbili. Hii IDA ndiyo yetu ya sisi masikini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko huyu Japan yeye voting powers zake 8.55% ana reserve kwenye Benki yake ya Taifa tani 846. China ana voting power ya 2.25% ana reserve ya dhahabu tani 1,948. Wewe Tanzania kwa nini bado una sita? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini na Benki Kuu kwa nini bado mnasita? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Professor.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia sasa. Nimalizie kwa kusema kwamba lazima tuwe na hiyo na kuwa na hiyo ni lazima refineries zetu mbili zifanye kazi. Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba refinery mbili za dhahabu tulizonazo ya Geita inaweza ika- process kilogram 600 kwa siku ya Mwanza 480 kwa siku. Lakini Waheshimiwa Wabunge hizi refineries hazina dhahabu na huenda zitafungwa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utazidi kuwashawishi Waheshimiwa Wabunge kwamba kuna umuhimu wa kuunga mkono bajeti hii kwa sababu inaanza safari ambayo tulikuwa hatuna. Michango ya Wabunge wengine wamesema kwamba mjusi arudishwe, mjusi wetu, naomba niwapatie ufafanuzi kidogo kuhusu huyo mjusi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mjusi huyu dinosaur ameanza kupatikana kwenye dunia yetu miaka milioni 231.4 iliyopita na yeye ndiye aliyekuwa kiumbe muhimu kwa zaidi ya miaka 135 iliyofuata. Mjusi huyu ana uzito wa kilo kati ya tani 50 na tani 70, urefu wake unatofautiana, lakini anaweza kuwa na urefu ambao unalingana na ghorofa sita. Mjusi wetu yuko Humboldt Museum ambayo zamani ilikuwa Ujerumani ya Mashariki, mimi nilikuwa naishi Berlin ya Magharibi yaani Ujerumani Magharibi. Nimeenda pale mara nyingi, nadhani zaidi ya mara mia moja.
Waheshimiwa Wabunge, nataka kuwaeleza ukweli ni kwamba hatuna uwezo wa kumrudisha na hatuna uwezo wa kumtunza, huo ndiyo ukweli kabisa. Tunachopaswa kufanya ni kujadiliana namna ya kupata yale mapato tugawane na Serikali ya Ujerumani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri wengine ambao tunafahamu yote hayo, siyo kwamba majadiliano hayajaanza, majadiliano tumeyafanya nadhani hata miezi miwili nyuma, nilikuwa najadiliana na Balozi wa Ujerumani na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Ujerumani namna ya kuweza kupata hilo pato. Ndugu zangu ukitaka kujua kwamba hatuwezi siyo kwamba tunahitaji muda kufikia hiyo ngazi hiyo, ukienda kwenye museum yetu Nyumba ya Makumbusho hii ukiangalia na kuangalia museum zingine duniani, utaona kuna tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo huyu mjusi tunafahamu na hawa mijusi (dinosaurs) wako familia zaidi ya 15, hawapatikani kwetu tu wanapatikana dunia nzima ndiyo maana kuna Jurassic Park. Kwa hiyo, tumuombe Mheshimiwa Waziri na wengine ambao tuna-connections huko tuendelee na mjadala wa kugawana yale mapato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mgogoro wa wakulima na wafugaji. Ndugu zangu tulioongea hapa tumeona kuna mwingine anavutia wafugaji, mwingine anavutia upande wa wakulima, vitu hivi lazima tuvikubali. Miaka 50 ijayo watakaokuwa kwenye hili Bunge, tuliyoyajadili hawatayajadili kwa namna hiyo, kwa sababu tuna imani watakuwa na kilimo bora, watakuwa na ufugaji bora, hawatakuwa watu wanajadili ukubwa wa maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sayansi inakokwenda inataka eneo linalolingana na hili Bunge letu liweze likalisha Mkoa mzima kwa mwaka mzima, ndiko huko tunakokwenda sayansi inatupeleka huko, maana yake kuna C4 plants na C3 ambayo inatumia carbon dioxide nyingi, mimea inakua kwa haraka sana, mtu anavuna mara tatu, mara nne, mara tano. Sasa suala siyo eneo, hapa ugomvi wetu kwa wakulima na wafugaji tatizo siyo eneo, tatizo ni matumizi madogo sana ya sayansi, teknolojia na ubunifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Watanzania mwaka 1950 tulikuwa watu milioni 7.7, mwaka jana tumefika milioni 53.5, mwaka 2050 tutakuwa watu karibu milioni 138 eneo ni lilelile la ukubwa wa 0.97 square kilometers million. Sasa tatizo hapa siyo maeneo, tatizo ni deployment of science, innovation na technologies ndiyo tatizo. Kwa hiyo, bajeti ya Mheshimiwa Profesa Maghembe tuipitishe tujipange kutumia sayansi na ubunifu zaidi kuliko kugombania ukubwa wa maeneo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia takwimu zinavyoonesha, kilimo chetu cha pamba hekta moja Tanzania tunatoa kilo 147, Malawi kilo 269, China kilo 1,524, Brazil kilo 1,530 hapa tatizo siyo eneo. Kwa hekta moja mwingine anazalisha zaidi. Mahindi juzi Namibia ambayo ni jangwa wamefikisha tani 11 kwa hekta moja, Tanzania bado tuko chini kabisa. Mihogo nchi ya Niger ni nchi jangwa kabisa, Niger wao wanazalisha tani 22 za muhogo kwa hekta moja, Tanzania tuko chini ya tani 10. Hivyo, Waheshimiwa Wabunge tatizo hapa siyo maeneo tusimalizane, tatizo hapa ni utumizi mdogo wa sayansi, teknolojia na ubunifu, kwa hiyo Mheshimiwa Maghembe bajeti yake tuipitishe tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maziwa, hawa ng‟ombe tunaowapigania wafugaji hatuna ng‟ombe wazuri. Nimechukua aina mbili tu za ng‟ombe wanaojulikana duniani kwa kutoa maziwa mengi. Mmoja anaitwa holstein yeye anatoa lita 11,428 kwa mwaka, wa kwetu hapa mzee sijui lita ngapi, Mheshimiwa Nsanzugwanko wewe ndio unafahamu mfugaji.
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hata tatizo kwa wafugaji hapa siyo eneo, tatizo ni sayansi, technology na ubunifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nyama hapa, tatizo siyo kumtengea mtu pori la kuwinda, mnyama wa kileo hii yaani tukichukua ng‟ombe, unapaswa kumfuga afikishe kilo zaidi ya 500, nyama anayoweza kuitoa bila mfupa, bila makongoro, bila nini ni kilo kati ya 340 na kilo 360. Kwa hiyo, ndugu zangu hii Wizara tuipatie bajeti, sisi wenyewe tujue kwamba matumizi yetu ya sayansi ni madogo, ndiyo maana tunagombania maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia fursa hii. Kwanza kabisa mimi nadhani nimpongeze Profesa anawizara ngumu ameuikuta pagumu anajitahidi enedelea kujitahidi, anajitahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kawaidia mimi natoa ushauri cha kwanza Profesa, hebu ile VETA ya Musoma Vijijini, na nilikueleza ukinipatia mimi VETA itakuwa ni ya mfano nchini; kwa sababu sitaki VETA ya mambo ya hoteli ya kutengeneza magari, hapana, mimi VETA yangu itakuwa mambo ya kilimo uvuvi na ufugaji. Naomba hiyo homework Profesa imalizie.

Mheshimiwa Spika, sasa Waheshimiwa Wabunge mimi natoa ushauri ifuatavyo. Elimu yetu, nilikuwa sipo, nimesikiliza, na ukweli ni kwamba iko kwenye hali mbaya, lazima kwanza tukiri hivyo. Lakini hakuna wa kulaumu, ni sisi wote. Tukitaka kumlaumu mtu ni kama hatujui tunalolifanya.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa muda umefika wa kujiuliza na pendekezo langu ni kwamba elimu ya awali kuipeleka TAMISEMI, imekaa TAMISEMI kwa muda matokeo yake siyo mazuri. Kama inawezekana, maana huko nyuma tulivyopeleka madaraka ya ndani si ndiyo tulifanya mabadiliko? Sasa tukifanya evaluation mabadiliko hajazaa matunda. Kwa hiyo mimi napendekeza, kwa sababu tumerudi nyuma Wizara ya Elimu irudishwe tena. Yaani mambo ya elimu yawe ndani ya wizara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inakuwa ngumu sana eti shule za msingi primary zinakuwa na Waziri wake na Ofisi zake ikifika university nayo na ya kwake halafu baadaye mnamlaumu huyu wa juu, mnamuonea, mnamuonea. Kwa hiyo mimi napendekeza Profesa lipeleke kwenye cabinet, mwambie PM alifikirie, uwe na wizara inaitwa Wizara ya Elimu, Sayansi Utafiti na Ubunifu Ministry of Education, Science, Research and Innovation. Huna haja ya kutaja teknolokjia, teknolojia kwa sababu innovation maana yake una innovate kwenye technology, kwa hiyo huna haja ya kuitaja. Hilo ni pendekezo langu la kwanza, tukifanya hivyo tutona mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni miundombinu kwenye mashule yetu. Profesa wewe na TAMISEMI, yaani wizara mbili lazima mkae chini mkubaliane kwamba, ili tuwe na elimu iliyo nzuri na inaweka msingi mzuri lazima kila shule; vyumba vya madarasa sawa lakini ni wanafunzi wangapi? Kwa hiyo, homework yako ya kwanza na wahusika turudi nyuma tuone kama tutarekebisha. Huko nyuma enzi yangu Waheshimiwa Wabunge shule ya msingi tulikuwa 45, sekondari tulikuwa 35, high school tulikuwa 25. Sasa hebu turudi huko kwanza. Hii mitaala hata ukiwa nayo mizuri namna gani ikiwa wanafunzi wamerundikana madarasani hautafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shule yoyote inayoitwa shule duniani kote; na mimi nimezunguka kwelikweli duniani hapa; sijawahi kwenda shule nikakuta shule haina maabara haina maktaba, hiyo ni shule gani? Mimi sasa hivi Musoma vijini shule za msingi tatu nimeweza kujenga maktaba. Na watu wananishangaa, wanasema Profesa mbona unang’ang’ana shule ya msingi iwe na maktaba? Nikasema kama unaona watu hawaelewi ushibishane nao sana, inabidi ukae kimya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba wanaoshughulika na elimu wahakikishe kwamba kila shule ina maktaba. Maktaba kwa nini, kwa sasa hawatahitaji vitabu? lakini maktaba zile tunakoenda tutaweka kompyuta zenye capacity kubwa na spidi kubwa; hata vitabu vingine mnavyovinunua sasa hivi vinatolewa bure, sasa kama hauna hizo kompyuta ndiyo maana ya hizi library lazima ziwe na computer, hata kama vitabu ni vichache mno, kusudu waweze kupata vitabu vya bure ambavyo sasa hivi vinagawanywa duniani.

Mheshimiwa Spika, lazima shule iwe na maabara, sekondari zetu zote lazima ziwe na maabara, hilo ni tatizo. Kwa hiyo ninaomba hayo yarekebishwe hayo. Kingine ninachokuja sasa nije kwenye mambo ya juu, Profesa haya yanakuhusu wewe na wengine wengine, nije Elimu ya Juu kidogo, na nilishapendekeza hapa.

Mheshimiwa Spika, hiyo COSTECH tuliyonayo hata tukimwaga humo fedha muundo wake COSTECH imekuwa kama idara ya Wizara. COSTECH haipaswi kuwa hivyo, inapaswa kwanza jina la COSTECH libadilishwe, iitwe National Research and Innovation Foundation. Iweke mkazo kwenye utafiti na mambo ya ubunifu, halafu na yenyewe ianzishe kufanya rating ya wasomi. Unajua haiwezekani, Maprofesa hawalingani jamani, au ma-Dkt. wote hawalingani. Sasa kwa kuwa hatuna rating hakuna Profesa wa grade “A" Profesa wa grade D, hakuna Dkt. wa grade A, grade D, kila mtu anaruka tu na title. Mimi Profesa, mimi Dkt., sasa inabidi wengine wale halali wakae kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hii kazi hii ni lazima tuiachie National Research and Innovation Foundation na duniani kote foundations ndio zimefanya vizuri. Uende Marekani, uende South Africa, uende wapi na wanapata fedha wanakuwa na watu wengi, hapo mambo yetu yataenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, nije kwenye vyuo vikuu, hapa ndio naomba Profesa aache legacy kwamba hiyo Wizara ilikaliwa na Profesa. Ni lazima ainge kwenye kila chuo, tatizo letu moja sasa hivi ndio maana ukichukua vyuo vya Tanzania, vyuo vya Tanzania vyote hakuna ambacho kiko kwenye kumi bora ndani ya Afrika, hatumo. Inamaanisha kwamba utafiti kwenye vyuo vyetu umeenda chini.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri ni kwamba mimi bado napokea ripoti ya machapisho. Kila niki–check Tanzania naona hamna, tuko chini, hivyo, Mheshimiwa Profesa akae na Vice Chancellors wake, watu wameanzisha journals, majarida kwa sababu ya promotion na yatazidi kudidimiza elimu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku moja Mwalimu alitutembelea, nashukuru mimi nilisoma Dar es Salaam University, Chancellor alikuwa Nyerere, akaja pale alikuwa amezowea kuonana na wafanyakazi na mimi ndio nilikuwa naanza kazi. Akasimama mtu mmoja senior akasema Mwalimu hiki chuo kina upendeleo sana, mimi sijapandishwa cheo. Mimi sikujua Mwalimu anamfahamu vizuri kumbe alimpa scholarship kwenda kusoma Marekani. Kaongea kaongea Mwalimu akatujibu wote akasema, jamani mimi nilikuwa nadhani mtu anayekuwa profesa, ni kweli mnahakikisha kweli kweli kwamba uprofesa unamstahili, kama ni suala la mshahara si wapandishieni tu mishahara, lakini msiwape hizi titles kwa urahisi rahisi hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa vyuo vyetu vimefikia hatua hata idara zimekuwa na journals, hizo ni just for promotion. Sasa Mheshimiwa Profesa nimsaidie najua anayafahamu,

atakavyokaa na Vice Chancellors wake atamwambia kila Vice Chancellor aje na journal za chuo chake. Wakikaa kwenye meza na wote wakae sehemu ambapo kuna internet au na nini, anamwambia anaanza ku–check journal yake moja baada ya nyingine. Ambazo hazifai, nyingi hazitafaa kwa sababu mimi nimeshazifanyia utafiti.

Mheshimiwa Spika, kuna kitu kinaitwa citation index (CI), wanaonisikiliza andikeni CI, Citation Index au kingine kinaitwa IP (Impact Factor). Citation Index maana yake ni kwamba hilo journal, hilo jarida unalolitumia ni wangapi wanafanya rejea zao, wanaofanya utafiti. Profesa Mkenda akikuta zina– impact factor ya 0.05 nitamwomba tuje tuongee, nadhani hazipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudia 0.05, Impact factor au Citation Index, inamaanisha hizi journal wanazozitumia duniani hazijulikani, kwa hiyo ni zetu tu hapo, backyard journals, lazima azipige vita Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, mwisho, kuna maeneo matatu ambayo lazima tuwekee mkazo na lazima vitu viunganike humu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Profesa muda wako umekwisha.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, namalizia hako ka mwisho.

SPIKA: Nakuongezea dakika tatu umalizie.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tena unaona maprofesa waungwana, ahsante profesa. Ni hivi, jamani tulieni mtafanya anisimamishe, stop. Ni kwamba Profesa Mkenda kuna maeneo matatu lazima ayaanzishe akiwa kwenye hiyo Wizara, ni space science and technologies na hiyo ndio yanaingia mambo ya satellites na mambo ya nini. Lazima aanzishe research kubwa na elimu kubwa kwenye eneo la mbegu, seed science, lazima si tunataka kwenda kwenye kilimo? Hata hii space science ni kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kuna ambalo ni kubwa, non- sciences, non-technologies hata wale wagonjwa wa TB duniani wameacha kutumia vidonge vingi siku hizi wanachukua kidonge size kama ya unywele inatibu TB, huko ndio dunia inakokwenda.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kutoa pongezi kwa Waziri wa Fedha, Naibu na Wizara nzima ya Fedha kwa sababu wametengeneza bajeti ambayo ni ya mwaka mmoja lakini iko kwenye picha ya miaka mitano na iko kwenye picha ya dira yetu ya maendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyojadili hii bajeti usiichukue kama ni ya mwaka mmoja, lazima uone kwamba ni bajeti ambayo imeanza safari ya kwenda mwaka 2025. Kwa hiyo ikiwa kweli tumedhamiria kuwa nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 inamaanisha bajeti yetu lazima inapanuka, inakuwa kubwa na fedha nyingi zinaenda kwenye maendeleo na siyo matumizi ya kawaida na ndiyo shukrani zangu nazitoa kwenye hii bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema tunataka kuwa nchi ya kipato cha kati mwaka 2025 maana yake ni kwamba ukipiga hesabu, bajeti yetu sasa hivi ni vizuri nikiongea kwenye dola kwa sababu nalinganisha na nchi zingine, GDP yetu (Pato la Taifa) karibu kwenye bilioni 55, 56. Kama tunataka kuwa nchi ya kipato cha kati, mwaka 2025 tunataka bajeti yetu ambayo itaonesha kwamba GDP per capita (pato la mtu mmoja) litakuwa la dola 3,000 inabidi tuizidishe mara nne. Kwa hiyo hii bajeti ni kubwa kwa sababu ifikapo mwaka 2025 tukiwa nchi ya kipato cha kati ni lazima tuwe na GDP ambayo ni zaidi ya bilioni 200 tuzidishe mara nne bajeti ya sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi engines ziko nyingi sana, engine za kupeleka vitu huko mbele huko na engine mojawapo ni umeme, na ndiyo maana bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini imekuwa kubwa ni ya shilingi trilioni 1.23 katika hiyo bajeti asilimia 94 zinaenda kwenye maendeleo na ukichukua kwenye maendeleo asilimia 98 inaenda kwenye umeme. Hapo ndipo unajua bajeti ya Serikali iliyotayarishwa na Dkt. Mpango na wenzake imedhamiria kweli kutufikisha uko. Dalili za kusema kwamba fedha zinapatikana ni kweli zitapatikana, mwaka huu tunaomaliza mwezi huu, Wizara ya Nishati na Madini upande wa maedeleo tumeshapata asilimia 82 na REA - umeme vijijini tumeshapata asilimia 81.
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti yetu kwa hiyo ni kwamba umeme vijijini ndiyo itawatoa watu kwenye umaskini. Bajeti mliyoipitisha ya umeme vijijini imo ndani ya bajeti kubwa ya Serikali ambayo ni ya umeme vijijini shilingi bilioni 534.4, hii imeongezwa kwa asilimia 50 ya bajeti ya mwaka uliopita. Lakini Waheshimiwa Wabunge na Watanzania ni kwamba kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchii hii, na kuonesha hii Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kujenga nchi ya viwanda, ni kwamba umeme vijijini tutakuja kufikisha trilioni moja. Kwa sababu hii ni Serikali inayoaminika, hata wenzetu wanaopenda kutuchangia maendeleo na wao wanaweza wakachangia zaidi ya bilioni 500 na taarifa nitawapatia ndani ya wiki mbili kutoka sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hii bajeti inahakikisha umeme unapatikana, siyo umeme tu kusambaza, lakini hii bajeti ndiyo itatuhahakikishia kwamba vyanzo vyetu vyote tulivyonavyo vya umeme tunaanza kuzalisha umeme. Tumejipanga kuzalisha umeme kutokana na gesi asilia, makaa ya mawe, maji, sola, upepo, joto ardhi, mawimbi (tides and waves) na mabaki ya mimiea (bio energies). Hayo yote yako kwenye hii bajeti ya trilioni 29.5, kwa hiyo ndugu zangu Wabunge tusipoipitisha hii, tukiwa na wasiwasi nayo basi haya yote ya umeme hayatakuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, na hii bajeti uzuri wake ndiyo inakuja kutuhakikishia kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchi hii haya mambo ya umeme ambao unakatikakatika hii bajeti ndiyo nakuja kutoa suluhisho la kudumu. Tunajenga njia za kusafirisha umeme kutoka kilovoti 220 tunakwenda kilovoti 400.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, mimi ningependa kuzidi kuwashawishi kwamba hii bajeti siyo ya mwaka mmoja bali inaanza safari ya kutufikisha mwaka 2025 na kwenye hii bajeti ndiyo tumeweka miradi mingi ya usambazaji wa umeme na ni muhimu sana. Waheshimiwa Wabunge wengi mmelalamika kwamba kuna vijiji vimerukwa. Hii bajeti ndiyo ina mradi wa kushusha transfoma na kusambaza nyaya kwenye vijiji ambavyo vimerukwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, mmesema hii sekta ya nishati haijashikwa vizuri sana na Watanzania. Hii bajeti ndiyoina fedha za kuwawezesha wazalishaji wadogo wa umeme na wao waweze kuchangia kwenye umeme wa Gridi ya Taifa. Vilevile kwa upande wa kuboresha upatikanaji wa umeme, hii bajeti itatuwezesha kuibadilisha TANESCO kabisa itoke TANESCO ya zamani kuja TANESCO ya karne ya 21. TANESCO itakuwa na ushindani, lakini bajeti ya kubadilisha muundo, mfumo na utendaji unaolalamikiwa wa TANESCO uko kwenye hii bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaoenda huko kuanzia tarehe 1 Julai tunaweka taratibu za kisheria za kunyang‟anya TANESCO mamlaka ya yenyewe ndiyo inazalisha peke yake, ndiyo inauza umeme peke yake, ndiyo inasafirisha umeme peke yake.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, mimi nigependa bado kusisitiza kwamba ni muhimu sana hii bajeti tukaiunga mkono na istoshe tumekuwa na sehemu tunaulizia ni kwamba kwa mfano wengine wamesema fedha za CAG, fedha za nani, ukweli ni kwamba bajeti hii acha ianze kufanya kazi na mahali ambapo tutakwama tutarudi tena hapa Bungeni kurekebisha.
Meshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo hii bajeti ni muhimu na diyo itatufikisha mwaka 2025 ambapo GDP per capita yetu ambayo itatoka sasa hivi dola 945 GDP per capita mpaka kwenda dola 3,000 kama GDP per capital.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Kwanza nianze kwa kusema kuna mengine yalikuwa ni ya utawala, mengine ni ya
kibinafsi, mimi sitagusia mambo ya utawala kwa sababu tuna mihimili mitatu, siwezi kuja kujadili
mambo ya utawala Bungeni, nadhani si utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili. Labda ifahamike vizuri sana hii ya bei, mimi
ninawasiliana na Waziri, ninawasiliana na Mwenyekiti wa Bodi. Kwa hiyo, aliye na barua kutoka
kwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji au Mwenyekiti wa Bodi ya EWURA hiyo ndio anapaswa
kuileta hapa Bungeni, ndio mimi nawasiliana nao hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ninafanya vikao vingi sana na wafadhili, vingi sana. Ni
vizuri ukiwa na barua moja uje na barua 20 maana vikao vyangu na wao ni vingi mno.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuje kwa mambo ya msingi. Kuhusu magwangala, niseme
vilevile kwa kifupi, nina ripoti nimetoa ushauri kwenye kila tani kumi ya magwangala ndio natoa
gramu nne! Kwenye kila tani kumi natoa gramu nne! Na yale magwangala katika kuchambua
dhahabu, mgodini wametumia siodine na huyu anakuja kutumia mercury! Waheshimiwa
Wabunge ninaacha mfanye tafsiri wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeulizwa swali la capital gain kati ya BG na Shell. Ukweli ni
kwamba Shell hawajalipa capital gain, hata mchana huu nilimuita Vice President wa Shell
ametoka London, kujadiliana nao. Msimamo wa Serikali ni kwamba lazima capital gain ilipwe
kwa sababu iko kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uwazi wa mikataba. Tulishasema mara mia hapa kwamba
yeyote anayehitaji mkataba wowote ataupata, tutauleta kwa Spika na pale atapata sehemu
atasoma, atarudisha. Na niombe, labda kwa kuwa kwa Spika labda ni usumbufu sana,
Mheshimiwa yule Mbunge Jumatatu, saa 2.00 asubuhi nimewaambia TPDC waweke mikataba
yote wampe asome. Ndio uwazi huo, hakuna cha kuficha. Aende asomee pale TPDC. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ya kusema uzoefu wa nchi zingine kwamba mikataba
inawekwa wazi, Waheshimiwa Wabunge na ninyi ni wazoefu, hakuna nchi ambayo unakuta
mkataba umeandikwa kwenye gazeti. Na kama kweli mkataba unaandikwa kwenye gazeti,
basi tuanze na mikataba yetu sisi wenyewe tuliyonayo tuchapishe kwenye magazeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sheria na kanuni. Ni kwei tunachelewa kutengeneza kanuni,
sasa hivi kanuni mpya nzuri kabisa ni kwamba mgodi wowote unaoanzishwa mara moja
unaenda kwenye Soko la Hisa. Sasa malalamiko kwamba hatufaidi yamekwisha, na ile iliyoanza
zamani imepewa miezi sita.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndugu zangu wa Kahama, Tarime, nendeni soko la
hisa sasa hakuna kisingizio kwamba, hatufaidiki. Narudia, Kanuni inasema lazima asilimia 60
zikamatwe na Watanzania, twendeni soko la hisa. Unajua huku sasa twende kwa vitendo
Waheshimiwa Wabunge, kwa vitendo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ruzuku kwa wachimbaji wadogo. Ruzuku zipo, iko kwenye Ilani
ya CCM na hizi ni fedha za mkopo wa World Bank. Wengine walisema ooh, nilijadiliana na World
Bank kuhusu bei ya umeme! Nina mijadala mingi, mbona hii ya wachimbaji hawasemi? Fedha
zipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu TANESCO deni lake. TANESCO wanadaiwa, kama
alivyosema Mwenyekiti, zimeshavuka shilingi bilioni 820. Na mimi bado msisitizo wangu sikubali TANESCO ipandishe bei hata kama wengine wakizunguka na barua, msimamo wangu huo
unafahamika, kwa sababu hili deni la shilingi bilioni 320 hatujalichambua, hatuwezi kuangalia tu
wanasema uzalishaji wa umeme ni wa bei kubwa lakini hatujachambua. Mtu hajaniambia kwa
nini bwana fedha wa kituo kimoja ana hoteli 4 wa TANESCO, huyo nae tumchangie, tupandishe
bei, haiwezekani, haiwezekani! Au mtu ananunua lita 20 anaandika amenunua lita 50!
Zimewekwa gari zote za TANESCO tracking system, hata maruti, hata zilizo kwenye mawe, eti
tupandishe bei umeme! Narudia, haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwisho wa mwaka wanapeana bonus milioni 50,
utapandishaje bei kwa ajili ya bonus zao? Haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, umeme haupandi hata mtu azunguke, kwanza wote
wanafahamu, World Bank, African Development Bank, European Union kitu ambacho nilikuwa
napambana nao, sikubali umeme upande. Lakini ukiangalia ile action plan wanasema tarrif review, nayo ni kiingereza. Review
maana yake sio hacking, you can review and go down. Hizi document ukizunguka nazo ni tafsiri vilevile.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu. Tuongee cha maana
zaidi. Ni kwamba, tukitaka Taifa letu liendelee ni lazima FDI (Foreign Direct Investiment) za
kutoka nje tuzivutie kutoka za sasa hivi 2.5 mpaka zaidi ya 15 ifikapo mwaka 2025. Na kufanya
hivyo kati ya mwaka huu na mwaka 2020 tunahitaji investment kwenye umeme; tunahitaji dola
bilioni 12. Alichosema Bashe ni muhimu 12 billion ikifika mwaka 2020 wakati tutakuwa na
megawati zaidi ya 5000. Na ndiyo maana tunaibadilisha TANESCO iwe ya kisasa na itaumiza
wenye biashara huko wanachukia lakini lazima ibadilike, iendane na haya matakwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema mengine ya muhimu sana kwamba
hatujafaidika na gesi, umeme tunaoutumia hapa mwingi ni wa gesi na kitakachotupeleka nchi
ya kipato cha kati ni uchumi wa gesi. Tuna mradi mkubwa wa LNG, tunaujadili, utachukua
muda utakuja hapa Bungeni. Tuna bomba la Tanga litakuja hapa Bungeni, kote tupo kwenye
matayarisho. Investment ya bomba la Uganda ni bilioni 3.5; lazima mtayarishe kabla hamjaanza
ujenzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, investment ya Liquefied Natural Gas (LNG) ya Lindi ni 30 billion
US Dollars; wapo kwenye matayarisho. Juzi nimetoka Zambia tumeleta tena mradi mwingine
mkubwa, bomba lingine tena; hii ndio maana inaitwa nchi ya mabomba mzee ambao
utakuwa karibu wa dola bilioni mbili. Sasa hii unaweza usione kitu kinafanyika, hii ni lazima ninyi Waheshimiwa Wabunge mje hapa, miradi hii inataka sheria, watu wamejifungia huko sasa hivi
hatulali mchana na usiku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha mbolea Mheshimiwa aliesema tunajenga
viwanda viwili, kimoja Kilwa na kingine Lindi. Cha Kilwa investment yake ni bilioni 1.9...
(Hapa kengele ya pili ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Kamati na Waheshimiwa Wabunge, naunga
mkono hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nadhani wasemaji wengi tumechukua mawazo yenu, suala ni umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya hiyo, nadhani kuna hivi viwanda vya mbolea cha Mtwara na cha Kilwa. Ukweli ni huu, tender ilifanyika, Ferrostaal ya Kilwa ikashinda tender. TPDC ikaanza kufanya kazi na kampuni iliyoshinda tender. Kampuni iliyoshindwa Helm ikaamua kufanya taratibu zingine kwenda kujenga kiwanda Mtwara, huo ndiyo ukweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali ya hayo yote sisi hatujatenga kampuni yoyote, niseme tu kwamba tulikaa kikao na Makamu wa Rais, nikapeleka wataalam wangu Mtwara, viwanda vyote vinapewa gesi, sitaki kwenda zaidi ya hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda cha Mkuranga Goodwill cha vigae, mitambo mabomba yamefika, yeye aliyekuwa anaomba gesi hajamaliza kujitayarisha na yenyewe ninaiachia hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la umeme, Waheshimiwa ni kwamba umeme tukubaliane kwamba popote duniani ukitaka kuanza kiwanda sehemu zote duniani, ardhi inakuwepo, maji yanakuwepo, umeme unakuwepo na mambo ya usafirishaji. Tukiri kwamba saa zingine tunavutia watu wanajenga viwanda wakati hivyo vitu vyote vitatu havipo. Kwa hiyo, siyo sahihi kusimama na kuanza kusema Wizara hiyo na hiyo lakini wakati unaenda kujenga kiwanda hukuiuliza Wizara. Japokuwa tuna majukumu ya kupeleka umeme pale, hilo nalo lifahamike hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kama tunavyojenga vyumba watu wanachelewa kutoa viwanja, watu wengine wanaenda kujenga milimani, halafu wanataka mabomba ya maji yaende milimani, umeme uende milimani, kwa hiyo ndiyo hali kama hiyo. Tujengea viwanda kwa mpangilio, badala ya kulaumu kwamba Wizara zina usingizi, katika Wizara inaheshimika dunaini ni Wizara ya Nishati na Madini. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme ni mtizamo naomba ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tuache mtizamo kwamba dunia ya leo umeme utazalishwa na TANESCO peke yake, haiwezekani. Kwa sababu nikiwapa hapa bajeti yaani makisio ya umeme kati ya mwaka jana na mwaka 2020 tunahitaji dola bilioni 11.6. Kati ya mwaka 2021 na 2025 tunahitaji dola bilioni 5.9, haya mahesabu yatakuja kama Wizara imelala?
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu power per capital twende tunapiga hesabu sasa, power per capital sasa hivi ni unit 138 kwa mtu kwa mwaka. Wakati tutaingia kwenye kipato cha kati mwaka 2025 tukiwa watu milioni 70 na GDP per capital ikiwa 3000 inaamanisha GDP yetu lazima iwe bilioni 211, power per capital lazima iwe zaidi ya unit 500 lakini ni bora ikawa 1400. Kwa hiyo, ndugu zangu nataka kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge huku Wizara ya Nishati na Madini tunaenda kwa mahesabu kweli kweli. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine hatutazalisha tu umeme ndani, ndiyo maana sasa hivi tumemaliza transmission lines, Mheshimiwa Rais akipata muda itabidi azindue, tumeongeza umeme mara mbili unaotoka Iringa, Dodoma, Shinyanga ndiyo maana umeme haukatikikatiki sasa hivi. Transmission line ile imetoka 220kv kwenda 400kv. Unataka matayarisho gani zaidi ya hayo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu tunajenga transmission line kubwa vilevile, mmeona kutoa Singida, Arusha kwenda Kenya, lakini hii ya Kenya, Kenya watajenga kilovolti 400 kuunganisha na Ethiopia, Ethiopia itaunganisha na Egypt n kilovolti 500. Tumeshaanza hata mahesabu ya kununua umeme wa bei ndogo kutoka Ethiopia. Duniani kote kuna kitu kinaitwa power trade hata ingekuwa na Mtanzania anatuuzia umeme wa bei mbaya miaka michache inayokuja hatutanunua. Umeme wa Ethiopia bei ya kwanza bado tunajadiliana nayo ni 7.5 US cents per unit, hatujasaini kwa sababu tutatumia miundombinu inayopita Kenya inaitwa willing charges hatuwezi kusaini hiyo mpaka tujue Kenya watatu-charge kiasi gani kwa unit.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huo umeme wa Ethiopia unaweza kwenda mpaka huku Zambia watautumia na sisi tutawa-charge, halafu tunajenga transmission line ya kutoka Tanzania kwenda Zambia tuungane na power pool ya Kusini. Hakuna usingizi Wizara ya Nishati na Madini hamna kitu kama hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu upande wa Kaskazini huku Bukoba sasa hivi wanatumia umeme wa Uganda ambao ni megawati 18. Ndugu zangu wengine wa Sumbawanga wanatumia umeme wa Zambia megawati Nne, Kenya wanaleta megawati moja. Sasa tunachokifanya na hivi karibuni tutaenda kuzindua ni Rusumo megawati 70 kwa nchi tatu, lakini tunajenga transmission line ya kutoka Rusumu kuja Nyakanazi. Wakati huo huo tunajenga kutoka transmission line kubwa kutoka Mbeya kuingia Sumbawanga mpaka Nyakazani, sasa haya nilivyosema ni mabilioni. Kwa mfano, transmission line kwa miaka minne ninahitaji dola bilioni 3.7. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, yote haya tunayafanya Wizara na Nishati na Madini tukiwa tunajua kwamba tunakuwa nchi ya kipato cha kati, lakini lazima uchumi ukue na uchumi kukua ni umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapinduzi ya uchumi (industrial revolution) mwaka 1746 yalichukua miaka 100 na yalihitaji vitu vitatu; yalikuwepo makaa ya mawe, chuma zamani ilikuwa ni viwanda vya pamba, baadaye ikaja revolution ya pili ndio ambayo ilienda kwenye mambo ya usafirishaji. Mapinduzi ya viwanda hayasimami, sasa hivi wakati sisi tunang‟ang‟ana na hivi viwanda vya chuma mapinduzi ya viwanda sasa hivi duniani ni non-technologies. Vitu ambavyo vina size ya unywele wako, ndiyo revolution iliyoko duniani sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hii ya kuweka solor panels inaanza kupitwa na wakati, majaribio yanafanyika Sahara watu wachukue umeme kutoka kwenye mchanga. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge nataka kuwathibitishia kwamba umeme wa uhakika utakuja na ndiyo maana napenda nirudie, ndiyo maana mimi nilikataa bei ya umeme kupanda kwa sababu huwezi ukajenga viwanda. Sasa niliyekataa bei ya umeme kupanda halafu eti nashtakiwa tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Profesa.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa tu ufafanuzi kwa mambo mawili yaliyoongelewa. Kwanza ni deni la umeme la Zanzibar; napenda kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge kwamba tunayo Kamati ambayo inaongozwa na Makatibu Wakuu wa pande zote mbili na wiki ijayo watakuja na nyaraka. Kuna maeneo wamekubaliana kuna maeneo hawakukubaliana. Kwa hiyo, nitaitisha kikao na mwenzangu wa Zanzibar ili jambo la deni la umeme tutalimaliza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la mafuta na gesi. Kwanza siyo limetolewa kwenye mambo ya Muungano, mimi mwenyewe nilikaribishwa kwenda Zanzibar wakati ambapo Sheria ya Zanzibar ya mwaka 2016 inazinduliwa na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar. Ambacho ni
muhimu na nimekisema mara nyingi, tusipende kuongea mafuta, mafuta, gesi, gesi nadhani cha kwanza kabisa tujue je, hayo mafuta yapo? Hiyo gesi ipo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kitu cha kuongelea hapa kwanza tujue kwamba kweli yapo au hayapo, hilo la kwanza. La pili, kama yapo, hiki kugawana siyo kitu ambacho ni kigeni duniani hapa. Sisi Tanzania tumeanza majadiliano kwa gesi au mafuta yaliyoko Ziwa Tanganyika lazima tukae chini na Kongo, Zambia na Burundi, hatuwezi kukwepa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huku chini Msumbiji ni lazima tufanye majadiliano na wenzetu wa Msumbiji tukienda kwenye vitalu vya kusini kabisa. Hiki siyo kitu kigeni duniani kinafahamika, kuna sheria za Kimataifa, kwenye Arctic Circle kuna mafuta mengi sana kule na gesi, inabidi Urusi na Ulaya wajadiliane. Kwenye mipaka ya Marekani na Canada kuna gesi na mafuta na wenyewe wanajadiliana. Nigeria na Cameroon wanajadiliana. Hivyo, ni vizuri exploration ifanyike upande wa Zanzibar tujue mafuta yako wapi au gesi iko wapi tukishapata ile ndiyo tutajadili namna ya kushirikiana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yako upande wa Zanzibar ni mafuta yao, kama yako upande wa Bara ni mafuta yao, lakini kama yako katikati hayakuheshimu mipaka ya kisiasa na ambavyo mara nyingi ndivyo inavyotokea, kwa sababu hivi ni vitu vilivyotengenezwa kati ya miaka milioni 55,200, Zanzibar haikuwepo, Bara haikuwepo hata Indian Ocean ndiyo ilikuwa inaanza kutengenezeka. Kwa hiyo, tuna taratibu za Kimataifa za namna ya kushirikiana kwenye rasilimali kama hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Zanzibar labda wanasiasa watalumbana sana lakini upande wa wataalam sisi tulitoa ahadi kuwasaidia wenzetu wa Zanzibar. Hata wiki jana badala ya kupeleka vijana Watanzania Bara 20 kwenda kusoma China mambo ya mafuta na gesi, kwa
kuwa nilitoa ahadi kwa Serikali ya Zanzibar nafasi tano tumepatia wenzetu wa Zanzibar waende kusoma kule China. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatoe hofu watu wanaosema mafuta kwanza, yakipatikana Magharibi mwa Pemba nachukulia mfano, huenda tusikwepe kujadiliana na Kenya. Kwa sababu ukiangalia mpaka wetu ukiuchora unavyokwenda huko juu kabisa ya Pemba, Pemba iko hapa, mpaka unapita hapa. Sasa kama mafuta yanaingia Kenya tutafanyaje? itabidi tujadiliane Zanzibar, Bara na Kenya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili jambo kitaalam ni la kawaida, wala msisumbuke ninyi tulieni. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, huwezi ukatenganisha viwanda na umeme. Umeme, tuna siku mbili; wiki ijayo, Alhamisi na Ijumaa, tunzeni maswali yenu yote, hebu leo tushughulikie viwanda tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa uagizaji wa makaa ya mawe kutoka nje. Kama unalipenda Taifa lako, ni lazima utapiga marufuku makaa ya mawe na gypsum yaani jasi isitoke nje. Twende kwa takwimu; ni kwamba tulikuwa na mtaalam mmoja tu, bahati mbaya amefariki Dkt. Semkiwa, alifanya Ph.D yake University ya Colon Ujerumani, Profesa wake alikuwa wa kutoka Australia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilikuwa wakati huo miaka ya 1990 wamepiga mahesabu kwamba tuna mashapo deposit ya bilioni tano ya ‘B’, ya baba. Miaka mitatu nyuma alivyoendelea na utafiti akasema, tunaweza tukafika bilioni kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unayesema turuhusu makaa kutoka nje, nawe tupatie takwimu za kuonesha kwamba hatuna makaa ya kutosha, lakini bila takwimu, msimamo wa Serikali ni kwamba bado tutazuia makaa yasitoke nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi, Ngaka walikuwa wanayumbayumba, wanazalisha tani 80,000 kwa siku; Magamba wanazalisha tani 1,000 kwa siku; Kabulo ambayo ni ya STAMICO wameanza tarehe 30 mwezi wa Nne sasa hivi wana tani 500. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, kama kuna mtu ana kiwanda cha saruji anakudanganya kwamba makaa hayapo, mwambie aje Wizarani kwangu aende Ngaka, aende Magamba, aende Kabulo, makaa ya mawe tunayo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu wa Lindi na Mtwara wamelalamika kwamba hakuna viwanda huko. Sehemu pekee kwenye Taifa hili kwa miaka kumi au ishirini inayokuja ambayo itaendelea kwa kasi, nasi wote tutahamia huko, ni Lindi na Mtwara. Mikoa mingine itabaki ni Mikoa ya kizamani; ya pamba, korosho, na dhahabu, mikoa ya kizamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi hakuna uwekezaji mkubwa ambao umeshafanyika wa kihistoria kama ambao utafanyika Lindi wa LNG; ni bilioni, bilioni, bilioni tena ya ‘B’; bilioni 30 ambayo ilikuwa inazidiwa na reli ya TAZAMA ikafuata bomba hili, inalofuata ni pale Likong’o Lindi. Utasemaje kwamba Lindi imesahaulika ina uwekezaji wa bilioni 30. Haiwezekani!

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua viwanda vikubwa vikubwa, hivyo vidogo namwachia Mheshimiwa Mwijage ndio anaviweza mwenyewe. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Kiwanda cha Mbolea kitajengwa Lindi tena mmoja nadhani sikuwepo, alitoa kauli mpaka Balozi wa Ujerumani amenipigia simu jana anasikitika sana, sijui alipata wapi taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaeleze, tuna viwanda viwili vitajengwa; cha mbolea cha Kilwa kitajengwa na Kampuni ya Ferrostaal. Hizi ni kampuni za Kimataifa na kile cha Mtwara kitajengwa na kampuni ya Helium nayo ni ya Ujerumani. Hayo ni makampuni ya Kimataifa, eeh! Sikiliza sasa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, hii ya Kilwa Ferrostaal Balozi huyu aliyemaliza muda wake kabla hajaondoka tunataka kwenda kuzindua groundbreaking ceremony. Siyo kuweka nini; ile tunaenda kabla ya tarehe 1 Julai, uwekezaji wake ni bilioni 1.92. Bilioni ‘B’! Utasemaje kwamba Lindi na Mtwara imesahaulika? Itazalisha mbolea Urea tani 2,200 kwa siku; Ammonium tani 3,850 kwa siku ya Urea. Utasemaje Mbeya wamesahaulika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu wa Mtwara, nitamwachia ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage aongee ya cement ya Dangote, lakini kuna kiwanda kingine cha mbolea cha Helium, haya ni makampuni makubwa! Nenda u-search u-google mwenyewe utayaona. Ni uwekezaji wa bilioni ya ‘B’ siyo milioni 1.26 na itazalisha tani 3,700 kwa siku. Utasemaje Lindi na Mtwara imesahaulika? Lindi na Mtwara ndiyo Mikoa mipya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme nimesema tuonane wiki ijayo. Nakuja suala la Liganga. Bado nina dakika tano! Niongeze speed eeh!

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanzoni wakati tunafanya utafiti, hatukujua namna ya kutenganisha iron, titanium na vanadium. Ph.D alifanya Profesa Mahinda, mimi nilikuwa bado mwanafunzi Dar es Salaam Chuo Kikuu, tulikuwa tunapigania chuma tu, lakini dunia sasa imebadilika, hii chuma haina thamani kubwa kuliko titanium na vanadium.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huyu mwekezaji kazi moja kubwa anayoifanya ni ya kutenganisha iron from titanium, from vanadium. Hiyo inataka muda, inataka vivutio; na hivi vivutio vinataka sheria zije humu zibadilishwe. Huwezi ukaweka vivutio kwa ajili ya Liganga na Mchuchuma peke yake, kwa hiyo, inamaanisha tupitie vivutio vyote; hata vivutio vilivyopo vya TIC uwekezaji wa umeme unahesabika sio strategic.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndugu zangu tukubali kwamba hatujachelewa na hii itafanyiwa kazi. Kingine ambacho ni muhimu ilikuwa ni mchuchuma, yaani kwenye makaa ya mawe. Wenyewe wakati wanatengeneza mradi, tulikuwa na matatizo ya umeme wakataka wauze senti 13 kwa unit moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mahesabu yao yote ya kuchimba chuma na makaa kuzalisha umeme, yalijikita kwenye senti 13. Kwa kuwa tuna umeme mwingi, huo sasa hivi tunauita umeme wa bei mbaya. Kwa hiyo, inabidi waje kwenye model ya senti saba au nane kwa unit. Hiyo model nayo inataka muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, msiseme kwamba vitu havifanyiki. Ameshafanya experiments kubwa sana za kujaribu kutenganisha iron, titanium, vanadium, lazima aje na model wa senti saba mpaka nane wa kuzalisha umeme wa Liganga. Kwa hiyo, Waheshimiwa ni kwamba kazi zinafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaoneshe, wenyewe tunataka kuzalisha tani milioni moja; vile vile tunabadilisha mawazo. Mawazo yalikuwa kuzalisha chuma kusafirisha nje ya nchi, lakini sisi ni kama wachezaji, ni kama tunachezea njugu. Wapo wasafirishaji wakubwa. Kwa hiyo, lazima tubadili concept hiyo. Kwa mfano, Australia mwaka 2016 chuma iliyozalishwa duniani, ilikuwa tani bilioni 3.4. Imewatosha?

Haya ahsante. Jamani hili la Liganga Mchuchuma, mwache, ni mambo ya kitaalam, linaenda vizuri. Ahsanteni. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Profesa Muhongo, ulikuwa unataja hapo hizo bilioni. Ni dola au ni hela za Kitanzania? Zote tu ulizotaja hayo mabilioni ni hela za Tanzania ama ni dola?

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilishawahi kuwaeleza, miradi yangu yote huku ni dola.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata hii nafasi. Kwanza kabisa nitoe pongezi kwa Serikali nzima ikiongozwa na Rais wetu kwa kazi nzuri na kutupatia Mpango wa kujadili. Pili, kwa sababu, hapa sipaswi kuongea mambo ya jimbo sana na Ndugu zangu wa Musoma Vijijini wanajua mambo yetu yanaenda vizuri kasoro barabara zetu ambazo nimeongea na TANROADS watabadili mbinu tuweze kupata lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yameongelewa, tunapaswa kutoa ushauri. Hapa napenda kutoa ushauri wangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayaongea haya ikiwa kama wahusika watapendezwa wataona yana uzito, basi wanaweza wakayaingiza kwenye mpango ambao wametuletea; kwanza kabisa wakati tunajadili hivi tujue hii ni sehemu ya Mpango ambao unatuelekeza mwaka 2025 tutakuwa tunakamilisha miaka yetu ile mitano ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambacho ni kikubwa sana tukifika 2025 tukiwa watu milioni 70 pato letu la Taifa linapaswa kuwa karibu zaidi ya bilioni 210 ikiwa kama pato la mtu mmoja mmoja kweli litafika dola 3,000 kwa mwaka, ndio malengo yetu hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tufike huko kwa kupitia huu mpango mimi nilitaka kwanza mpango wetu watakavyoenda kuutekeleza uwe na malengo. Malengo hasa ni nini tukiwa tunaelekea 2025 na hii ni transit period?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachotaka kuona kinawekwa msisitizo ni ukuaji wa uchumi, lengo kubwa hilo, growth. Tumeshuka nne, tutaenda tano, sasa tujitahidi kama tunataka kuondoa umasikini nchi hii tujitahidi uchumi uvuke asilimia saba na wanasema ukiwa asilimia nane duniani kote ndio umaskini unapungua. Ukiwa chini ya nane Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tujue umasikini bado una sisi. Tukitaka kwenda vizuri sana mpango tuuelekeze kwenye ukuaji wa asilimia 10 na zaidi ndio tutasema sasa uchumi unaenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la pili ni kuwafanya wananchi waishi kwa neema yaani wealth creation sijui kiswahili chake lile ni lengo la pili la muhimu sana. Lengo la tatu, kwenye huu Mpango ni suala la ajira tulipaswa kuelezwa ajira ndani ya mwaka huu mmoja tutatengeneza ajira ngapi? Na tunakoelekea 2025 tunadhani tutakuwa tunatengeneza ajira ngapi kila mwaka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne, ni huduma kwa jamii hayo sasa ni maji, umeme, barabara, hizo ni community service huu Mpango unapaswa kutueleza hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho sikukiona sijakisikia lengo letu tunataka shilingi yetu iwe kubwa, tuna gold refineries mbili mpya tumesema tuanze kuwa na akiba ya dhahabu gold reserve naomba huu Mpango nao useme kwenye huu mwaka unaokuja tutaanzaje? Tutaendaje kwa sababu sasa tuna refineries ambazo zinaweza zikasafisha dhahabu kufikia zaidi ya asilimia 99.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hayo ndiyo maeneo ambayo tunategemea yawe kwenye Mpango. Lakini nini cha kufanya kutekeleza hayo malengo nini cha kufanya cha kwanza kabisa kimeongelewa na kila mtu ni suala la kilimo hicho ndicho cha kufanya sasa wengi wameyaongea sitaki kurudia huko tena kilimo. Lakini tukisema kilimo tunachukua maana ya mifugo, uvuvi yote hiyo tunaweka kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili ni suala la elimu Taifa lote duniani kote hata mataifa yaliyoendelea kila mwaka yana mpango wa elimu na sisi tunataka tufate huu mwaka mmoja tutakuwa na shule ngapi mpya tutaajiri walimu wangapi tutakuwa na vyuo vitatoa wangapi? Mpango wa elimu lazima ujulikane uwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni afya tunajenga vituo vya afya tunajenga zahanati lakini kwenye Mpango useme kwamba kwa huu mwaka tunakuwa na zahanati kadhaa, vituo vya afya kadhaa, hospitali za rufaa kadhaa. Kingine ni miundombinu ambayo tumesema kamati ya bajeti naishukuru kwa staili ya kilometa tano tano, tatu tatu kila mkoa hiyo siyo mbinu nzuri ya kujenga barabara zetu. Lakini Mpango utueleze utashughulikaje na mambo ya miundombinu hasa mabarabara ya vijijini ambayo yanaenda kuleta mazao kutoka vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na cha muhimu zaidi Mpango uongelee mambo ya mazingira na tabia nchi ni vitu viwili tofauti environment and climate change ni vitu viwili tofauti mazingira na tabia nchi. Mpango sidhani kwamba umejieleza dunia inasema tushuke chini ya nyuzi 1.5 lakini sehemu zingine za Tanzania temperature raise inafika mpaka three degrees celosias kwenye Indian ocean imeshavuka 1% celosias mpango ueleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mpango sasa ikiwa hayo ndiyo maeneo na malengo, tutoe wapi fedha nadhani hiki ndiyo kitu muhimu sana financial resources cha kwanza ambacho Mpango unapaswa kuegemea kabisa na mapato mengi yatatoka kwenye kilimo na kilimo kama nilivyosema mwezi Februari lazima tuwe na priority hatuwezi kwenda na mazao yote kwa mpigo lazima tuchukue mazao ambayo yanahitajika duniani sasa hivi tuko karibu watu bilioni 8 na watu wanakula mchele kila siku wanatumia ngano kila siku wanatumia mahindi kila siku, wanatumia muhogo hayo mazao manne ndiyo ya muhimu halafu na mazao ya horticulture hayo matunda ma-avocado na nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu utueleze tutazalisha mahindi kiasi gani? Ngano kiasi gani? Mihogo kiasi gani? Na hiyo horticulture kiasi gani hatuwezi kuwa tunaongelea avocado hata haujui hauna projection kwamba utazalisha avocado kiasi gani. Chanzo cha pili cha fedha na bahati mbaya sana hakijajadiliwa watanzania naomba nizidi kuwasihi.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Professor muda tayari.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Nilikuwa naongelea mambo ya gesi economy, kutumia methyl kutumia helium nilitaka kuongea mambo ya mining kuingia kwenye madini mapya yanayotakiwa sasa hivi duniani especially hii gesi ya helium duniani sisi tukishindwa kuichimba wengine wameweka contracts wanataka kwenda kuichimba mwezini kwa hiyo ya kwetu tunaweza kuwa nayo tunajadiliana itabaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine nilitaka kumalizia hayo huko tunakokwenda ni kutafuta hizi fedha za climate fund halafu vile vile nilitaka kumalizia kwa kusema kwamba Mpango huu kitu ambacho hatujakipata pale ni yard stick tutapimaje tumefanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilitaka kusema ili tujue tumefanikiwa huu mpango utueleze tunapunguza umaskini kwa kiasi gani? GDP per capital inaongezeka kwa kiasi gani? Halafu watu wangapi wamepata kazi? Viwanda vingapi tumevijenga? Yaani hizo naongea kwa ujumla lakini hapa we need facts and figures wakati tutakuja ku-interrogate mafanikio ya mpango huu halafu gold reserve inatia huruma mtu wa kwanza mwenye gold reserve duniani ni Marekani nilishangaa kuona hata Malawi ina gold reserve niki-check Tanzania gold reserve ni zero huu mpango unatuelezaje ndani ya mwaka mmoja tukielekea 2025. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Professor ahsante sana.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kujenga viwanda vyetu vya mbolea Mpango utueleze tunajenga pale Kilwa Mpango haujasema tunajenga na Mtwara, ahsante.
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikupatie pongezi nyingi sana na nikutakie kila la kheri kwenye nafasi yako ya Naibu Spika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nichukue point moja tu ya kusisitiza kutoka kwenye Kamati yetu ya Kilimo. Kamati imetoa mapendekezo mazuri mno na yameandikwa vizuri mno, kwa dakika tano hizi naongelea kitu kimoja tu na ni kuishauri Serikali irudishe tena Tume ya Mipango na nitatoa sababu hapa kwa nini Tume ya Mipango ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Tume ya Mipango (Planning Commission) ipo chini ya Wizara ya Fedha ndiyo maana inaitwa Wizara ya Fedha na Mipango, lakini inakuwa ni kama Idara, sasa kama ni Idara ndani ya Wizara haina mtizamo wa Kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano wa Mkoa wa Mara kwa nini Tume ya Taifa inahitajika. Mkoa wa Mara viwanja vya ndege kuna kiwanja cha Musoma Mjini, mimi nimezaliwa pale Mjini, kiwanja nimekikuta wanakikarabati sasa hivi, kabla ya Baba wa Taifa hajastaafu kuna eneo limetengwa kabisa Nyasurura, Musoma Vijijini ilikuwa itengenezwe airport kubwa ambayo ingehudumia hata sehemu zingine za Afrika Mashariki na nje, kwenye Ilani ya Uchaguzi kiwanja hicho kimo, juzi sisi tumekabidhi Bodi ya Viwanja kwamba jamani chukueni kiwanja mjenge.

Kwa hiyo, Musoma Mjini tuna kiwanja, toka enzi ya Mwalimu tumekuwa na kiwanja kingine kikubwa, nadhani mmesikia Serengeti Mugumu na wao wanataka kuwana kiwanja, sasa kipi ni bora katika hivi vitatu ndani ya Mkoa mmoja?

Mheshimiwa Naibu Spika, inamaanisha tunaopanga hatuna picha kubwa ya Kitaifa. Unachukua Mkoa jirani wa Simiyu na wenyewe wanataka kiwanja, Mwanza kuna kiwanja, ndiyo maana Planning Commission ingekuwepo vitu kama hivi vingeliweza kushughulikiwa kwenye picha kubwa ya kitaifa umuhimu wa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano wa pili ni ujenzi wa barabara; tumeshauri TANROADS, huu mpangilio wa sasa wa kilometa tano/tano, Waheshimiwa Wabunge kila mtu ana furaha ana mradi wa barabara lakini kila mtu ajiulize utaisha lini? Mimi nina barabara ya kilometa 92 karibu kilometa 100, wamepewa kilomita tano, kwa hiyo muda mfupi kabisa kama pesa zinatakiwa kutoka ni miaka 20, lakini Planning Commission ingekuwepo ingeona ni barabara zipi ambazo ni muhimu kiuchumi badala ya kujenga kilometa tano/tano labda wangekuwa wanajenga angalau kilometa hamsini kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine ni mambo ya umwagiliaji; tunaongea kila mbunge hapa ana scheme yake lakini uwezo wetu wa kifedha hatuwezi kuwa na irrigation scheme kila Mkoa, kila Wilaya, hatuna ubavu huo wa fedha. Kwa hiyo, Planning Commission ingekaa ikaona ni yupi na wapi tuwekeze zaidi tuweze kuanzisha kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo, ukija kwenye ujenzi wa mambo ya vyuo vya VETA, kama nini Mbunge wa Musoma Vijijini sihitaji VETA ya kufundisha watu kutengeneza magari, ninahitaji VETA ya watu wa mifugo, kilimo na uvuvi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Profesa Muhongo.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja muda ungepatikana ningewaeleza zaidi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kutoa shukrani kwa Serikali, Jimbo la Musoma Vijijini linaridhika sana tunapata miradi na ni Jimbo pekee ambalo ukitaka mradi wako utekelezwe njoo Musoma Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani ya pili ni kwa Serikali kwamba, kuna wajanja-wajanja ambao hawakutekeleza miradi yetu vizuri sasa Serikali imeanza kutumia vyombo vyake kufanya uchunguzi. Nitoe pongezi Serikali kuamua kufanya uchunguzi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani nyingine ni ya kufufua mradi ulioanzishwa na Mwalimu, wote wameongea hapa kilimo cha umwagiliaji na eneo ambalo Mwalimu alikuwa amelitenga mwaka 1973/1974 aanze kumwagilia kwa hekta 2,500 kule Bugwema natoa shukrani kwa Mheshimiwa Rais alivyokuwa Musoma Vijijini tukamuomba kwamba, ule mradi uanze na ninadhani bajeti itakayosomwa ya kilimo itaelezea jinsi ambavyo Bugwema Irrigation Scheme itafufuliwa na ninadhani tutalisha Tanzania nzima na nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mbali ya hayo ya Jimboni nije kwenye hoja ya Waziri Mkuu, ambayo naiunga mkono. Mimi nitaongelea sehemu mbili kuhusu sera na ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sera. Kama Taifa inabidi tuwe na sera nzuri sana ya mambo ya utafiti, maendeleo ya utafiti na ubunifu (Research Development and Innovation). Yote tunayoyaongea haya tukitaka kufanikiwa lazima tuwekeze kwenye utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano mwaka 2020 nchi ambayo ilitumia pesa nyingi kwenye utafiti ukilinganisha na GDP yao ni Belgium na Sweden, ndiyo zilitumia asilimia
3.5. Nchi za Kiafrika mwaka 2006 tulipitisha kule Sudan Azimio kwamba, angalau tutumie asilimia moja ya pato letu la Taifa kwenda kwenye utafiti. Nchi nyingi za Afrika hazijafika huko, waliokaribia ni South Africa, Kenya na Senegal na wako 0.8 Tanzania tuko 0.5. Kwa hiyo, ninaomba kwa ajili ya sera na ofisi ya Waziri Mkuu kwa sababu ndiyo inachukua kila sekta hii tuongeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo 0.5 nadhani haijatoka kama ipasavyo, maana yake tukichukua GDP yetu kama sasa hivi ni Dola tuseme Bilioni 60. Ukichukua asilimia Moja ya hiyo, karibu ni Dola Milioni 650, ukichukua 0.5 ni zaidi karibu Dola Milioni 300, sidhani kwamba, tunatumia. Maeneo ambayo tunapaswa kuweka mkazo kwenye sera ya utafiti, nimechukua ni maeneo matano na Kiswahili chake wataalam watakuwa wanatafsiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza ni mambo ya space science na technology. Tunataka kilimo bora, lazima tujue mambo ya space science. Tunataka uvuvi, tunataka utalii, lazima twende kwenye space science na technology. Wengi wakisikia space wanadhani ni kitu kikubwa sana kinatisha, hapana! Tunahitaji kuwa na satellites.

Mheshimiwa Naibu Spika, sikilizeni ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, Kenya wana satellite, Uganda watarusha moja mwaka huu, Zambia watarusha mwakani moja, Rwanda wanayo moja, Egypt wanazo tisa, Nigeria wanazo saba. Kwa hiyo, kwenye mpango wa utafiti na vyuo vyetu lazima tuanzishe degree programs ambazo zinajielekeza huko kwa sababu, satellite siyo kitu cha ajabu, tunahitaji kwenye mawasiliano na hata kwa mambo yetu ya hali ya hewa na madhara mengine ambayo yanaweza yakatupata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni haya maeneo ninayoyataja karibu dunia nzima imeweka macho hapo ni life sciences, mambo ya kilimo, mambo ya mazingira, lazima tuwekeze kwenye life sciences.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni nuclear sciences. Nuclear siyo kwa ajili tu ya kutengeneza mabomu, lakini vifaa vingi sana vya hospitali vina nuclear science na technology ndani yake. Eneo hili hatujawekeza, lazima vijana wetu tuanze kuwasomesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la nne ni environmental sciences. Wengi wameongea, mazingira hata yale ya Mto Mara tungekuwa na wataalam wengi yasingetupata yaliyotupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho la tano, kama tuna fedha zinatosha basi tuweke kwenye artificial intelligence. Hilo ndiyo eneo jipya ambalo tunakwenda, lakini tukitaka kufanya hayo pendekezo langu moja kubwa na ninaomba nilirudie ni lazima ile COSTECH ibadilike, COSTECH isiwe idara ndogo ni lazima tutengeneze kitu kinaitwa National Research and Innovation. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ile COSTECH tuibadilishe iitwe National Research Foundation and Innovation. Mambo yetu yote tunayoyataka ya utafiti na wapate hizi fedha ambazo tunazipigia hesabu, Mamilioni ya Dola.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nilipenda kuchangia ni ajira. Wengine wote wameelekeza hukohuko kwamba, Tanzania kama tunataka kutoa ajira siyo ya kuajiriwa Serikalini, hatutaweza. Saa hizi tuko watu karibu Milioni 65 wanaoajiriwa hawajafika hata Milioni Moja, mahali ambapo watu wataajiriwa ni kwenye kilimo, kwenye uvuvi na ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huko tunakotaka kwenda ni kwa sababu sasa hivi duniani tuko watu karibu Bilioni Nane na hesabu imepigwa kila mwanadamu anahitaji chakula kwa siku kinachokwenda kwenye kilo 1.4. Kwa hiyo, tulime mazao ambayo tutaenda kuyauza huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia mazao yanayopendwa, vyakula vinavyopendwa duniani ni 12, nitavitaja kwa haraka haraka; salad, chicken , cheese, rice tea, coffee, milk, eggs, apples, soup, yoghurt na bread.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ndivyo vyakula vinavyopendwa sana duniani. Vyakula vyote hivi tuwe na mpangilio wa kuzalisha kuuzia dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ili tufanye hivyo tunahitaji kuwa na kilimo cha umwagiliaji kama ambacho tutakuja kufanya kule Musoma Vijijini kwenye Bonde la Bugwema. Lile bonde ni kubwa ni zaidi ya hekta 10,000. Kwa hiyo, turudi pale Mwalimu alipotaka kuanzia, hebu tuanzie hekta 2,500 halafu viwanda tunavyovijenga ni lazima viwe viwanda ambavyo vimejiegemea sana kwenye mazao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu tunaolima pamba tungetaka kuwa na ginneries, tulitaka kuwa na viwanda vya nguo, ambao tunafuga kama kule kwangu Musoma Vijijini na Mkoa wa Mara tunataka tena tuanze kuwa na viwanda vya maziwa na cheese na butter kama ambavyo dunia inahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukienda kwenye kilimo nashukuru sana hawa vijana wa magwanda kweli wanachapa kazi, lakini lazima tushindane na wakubwa. Nimechukua hapa takwimu zinaonesha namna ambavyo wale wakubwa wanalima na sisi tujaribu kwenda angalao hata asilimia 10 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukichukua mchele China inaongoza duniani inazalisha tani milioni 150, Tanzania tujipime.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimechukua ngano China ya kwanza. Karibu mazao mengi ni wachina.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, hiyo ni kengele ya pili, malizia kwa sekunde tatu.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sekunde tatu; ni kwamba, tujitahidi hata wanigeria tuwazidi kuvuna mihogo ambao wao wana tani milioni 60 sasa Tanzania angalau tufikishe tani milioni 40. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nadhani nina dakika kumi, kwa hiyo, nitakuwa na kengele mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni hivi, kwanza kabisa huyu Mbunge ambaye amemaliza kusema nitumie dakika yangu moja kuwasaidia wanaopanga mambo ya madini. Tanzanite tulijaribu kuweka Centre kubwa iwe Arusha na tukaweka mitambo ya kuchonga na kuongeza thamani. Sasa ukisema madini yale yasiende Arusha, basi ile mitambo ya gemology yote inakuwa redundant. Ni hilo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa kwanza kabisa kwenye hii Wizara, naunga mkono tupitishe bajeti, wafanye kazi. Kama kawaida yangu, mimi natoa mawazo mapana zaidi. La kwanza ni kwamba, naomba hii Wizara ifanye kazi na Benki Kuu na tuweze kuanza kuwa na gold reserves. Maana ya kuwa na gold reserves, yaani kutunza dhahabu kwenye Benki Kuu yetu, kwa sababu kubwa tatu. Kwanza kunaimarisha sarafu yetu ya shilingi, halafu inasaidia mfumuko wa bei, na tatu ndiyo reserve ambayo inaaminika haina risk ya aina yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuthibitisha hiyo point, angalieni wakubwa duniani reserves walizonazo. Wa kwanza ni Mmarekani dunia nzima ana gold reserve tani 8,133; wa pili ni Mjerumani, ana reserve ya gold tani 3,359; wa tatu ni Italy; wa nne ni France; wa tano ni Urusi, ana tani 2,302; na wa sita ni China, ana tani 1,948. Sasa hawa wakubwa ambao wana uchumi mkubwa, wanalinda uchumi wa nchi zao kwa kuwa na gold reserves, kwa nini sisi Tanzania tusifanye hivyo? Hilio ndilo pendekezo na ombi langu la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa linganisha na nchi zinazotuzunguka. Msumbiji ambao tunawazidi uchumi, wana gold reserve ya tani 3.94; Burundi ambao tunawazidi, reserve yao ni 0.03 tons; Kenya ambao wanatuzidi uchumi, wao wana reserve ya 0.02 tons. Kwa hiyo, ni kwamba kwa kuwa tunakuwa na refinery nzuri sana kule Geita ambayo tutaweza kufanya purification ya gold kufikia 99.99. Kwa hiyo, ni muda muafaka sasa sisi kuwa na gold reserves zetu. Pendekezo langu la kwanza hilo.

Mheshimiwa Spika, la pili, tumeambiwa kwamba, baada ya Covid kuja sasa ndiyo tunapata takwimu sahihi. Wanasema uchumi ulishuka ukafika 4.8, sasa tuko 4.9. Ni lazima turudi seven twende eight na ikiwezekana ten percent.

Ndugu zangu Watanzania, uchumi usipokua kwa kadiri ya kiwango cha 8%, 10%, 10% na kuendelea hatuwezi kufuta umasikini nchini. Kwa hiyo, kitu kitakachotusaidia hapa ni kwenye sekta za uzalishaji muhimu; kilimo, uvuvi na ufugaji. Kingine ambacho kitatusaidia, ni lazima twende kwenye uchumi wa gesi, tupende tusipende, twende huko. Cha tatu, ni kwenye madini sasa. Haya Mheshimiwa Waziri ameyasema, sawa, tuendelee; ni dhahabu, vito na gemstones, lakini kwa miaka 20 inayokuja hapa duniani, madini yanayotakiwa hatujaanza kuyachimba sisi. Kwa hiyo, geological survey aliyokuwa anaiongea, tuipatie hii kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, geological survey ya Dodoma kabla ya mwaka 1961 wa Uhuru, ndiyo ilikuwa geological survey kubwa ambayo nchi nyingine walikuwa wanaleta watu wao kufanya mafunzo hapa. Tuiwezeshe hiyo. Geological survey kwangu mimi ni muhimu kuliko hii Tume ya Madini, ni muhimu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa madini ambayo tunapaswa kuyashughulikia kwa ajili ya kutoka 4.9% twende 8% economic growth rate, twende 10%, twende kwenye helium. Sikumsikia Waziri anaongelea helium gas. Hii gesi haiko Nishati. Kwa taratibu za nchi yetu, helium inasimamiwa na Wizara ya Madini, kama sijakosea. Sasa hivi hii helium ambayo iko nyingi huko Rukwa, global demand, duniani zinatumika six billion cubic feet. Duniani wanahitaji six billion cubic feet of helium per annum na growth yake itafika mpaka 10%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka kesho soko la helium litakuwa na thamani ya 16 billion US Dollars na mtumiaji mkubwa ni NASA, anatumia 100,000,000 cubic feet per annum.

Kwa hiyo, naomba twende kwenye helium tuiendeleze. Hata hivyo, na yenyewe itakuwa kama ile ya LNG amabyo inabidi tuipeleke kwenye kimiminika (liquid). Tui- liquefy ile kule Lindi mpaka kwenye temperature ya -161.5, hiyo ni LNG, lakini helium ya Rukwa ni lazima tui-liquefy iende -2.69 degrees celsius. Haya siyo mambo ya mzaha. Minus! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa madini yanayohitajika duniani yatatumika kwenye magari, kwenye aerospace, military, clean energy na fourth industrial revolution. Wachina wamesema kufika mwaka 2025 wanataka kuachana na magari ya mafuta, wanahitaji madini. Madini ambayo yatahitajika kwa miaka 20 inayokuja, naomba niyataje; ni cobalt, chromium… (Makofi)

Aah, msipige makofi yasikike vizuri. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni cobalt, chromium, lithium, palladium, nickel, zink, manganese, gallium, germanium, indium. Halafu na hii platinum group elements pamoja na rea earth elements. Kwa hiyo, naomba tukawekeze huko. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, madini mengine ambayo tunapaswa kuwekeza ni ya kutengeneza mbolea. Tunasema mbolea, mbolea; geological survey ipewe kazi ya kutafuta madini mbali ya natural gas, lakini kuna madini mengine kama potassium salts, kama ile ya Minjingu Phosphate, ni kazi ya madini hii.

Mheshimiwa Spika, kingine ambacho tunapaswa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga. Ahsante sana.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, haya ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, nadhani sasa tutulie tupate mambo mengine tofauti kabisa na hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utazidi kusisitiza umuhimu wa ukujuaji wa uchumi wa Taifa hili. Baadaye mtaona nitasisitiza umuhimu wa Sekta ya Uvuvi kwa ajili ya ukuaji wa uchumi wa Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, nikianza na Jimbo langu la Musoma Vijijini, tuna kata 21, tuna vijiji 68, Kata 18 ziko pembezoni mwa Ziwa Victoria wanajishughulisha na uvuvi. Katika hizi kata, ni kata tatu. Kwa hiyo, hiki ni kithibitisho kwamba uvuvi lazima uchangie uchumi wetu kwa hali ya juu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uvuvi tunavyouchukulia sisi watu wa Musoma na nadhani ndiyo Taifa zima, kwanza unatoa chakula. Kwa hiyo, kwa mambo ya kiuchumi, uvuvi ni kwenye food security, uvuvi unatoa ajira na uvuvi unachangia uchumi wa mtu mmoja mmoja na uchumi wa Taifa. Uchumi wa Tanzania kwa muda wa kama miaka mitatu, minne unakua kati ya asilimia tano na sita. Saa hizi nadhani upo kwenye 5.6.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwenye hili Bunge la Bajeti kuna maeneo ambayo ninawasihi tutoe ushauri kwa Serikali kusudi uchumi wetu kama tunataka uondoe umasikini kama nilivyowaeleza juzi, uchumi ni lazima ukue kuanzia asilimia nane kwenda asilimia 10. Ni sekta tano tu ndizo zinaweza kufanya uchumi uende kwa haraka (accelerated growth). Cha kwanza kabisa ni gesi asilia. Tutalijadili huko. Cha pili ni madini, cha tatu ni kilimo, inakuja mifugo na uvuvi na cha tano ni utalii. Hizi sekta tano, kila moja ningechangia asilimia mbili ya ukuaji wa uchumi, tungeweza kufika hizo nane mpaka kumi.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa nini nasema uchumi. Wataalamu wa lishe wanasema kwamba, kama unataka balanced diet (chakula bora) unapaswa kutumia grams 280 mara mbili kwa wiki. Yaani portion ya kwanza gramu 140, na siku nyingine gramu 140, 280. Sasa tunavyosema uvuvi ni uchumi muhimu, tuangalie soko letu kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, soko letu la kwanza, kama wananchi wote duniani wanataka kula namna hiyo, wako watu bilioni nane sasa hivi. Tanzania ikiuza huko Samaki, tutapata fedha nyingi. Kama soko letu ni ndani ya Bara la Afrika, sasa hivi Barani Afrika tuko watu bilioni 1.43. Kwa hiyo, hizo ni fedha nyingi sana ukipiga kwa grams 280. Kwa hiyo, Sekta ya Uvuvi tuichukulie kibiashara.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2022 samaki waliozalishwa duniani walikuwa ni tani milioni 184.6. Mzalishaji wa kwanza hapo alikuwa ni China aliyezalisha tani milioni 67.5, na katika hizo tani milioni 54.6 alizalisha kutumia vizimba, na huko baadaye ndiyo nitakuja kusisitiza suala la vizimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wa pili alikuwa ni India ambaye uzalishaji wake duniani ni asilimia 7.56. Sasa maoteo ya mwaka huu ya biashara ya samaki duniani, mapato yake yatafika bilioni 612. Hapo ndipo tunapaswa kushawishi na kuishauri Serikali iwekeze zaidi kwenye uvuvi. Samaki wa vizimba duniani wanaozalishwa ni tani milioni 180. Mzalishaji namba moja ni China, anazalisha theluthi moja; wa pili, ni India ambaye anachuana na Misri (Egypt). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa Afrika Egypt ndiyo inaongoza, sasa Egypt yenyewe kwa mfano mwaka juzi ilizalisha samaki tani milioni 2.2 kati ya hizo, tani milioni 1.7 walizalishwa kupitia vizimba hii ni zaidi ya 77%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hoja yangu hapa na mchango wangu kwenye hii Wizara nitabaki kwenye uvuvi na ninazidi kusisitiza umuhimu wa samaki wengi wamesema samaki wamekosekana Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa na Ziwa Victoria. Suluhisho lake ni samaki uvuvi wa vizimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuiangalie Tanzania ilivyo na ndugu zangu wa Lake Tanganyika walikuwa wanalalamika, wana haki ya kulalamika. Utafiti ambao nina muomba Mheshimiwa Ulega na maprofesa wake wafanye siyo ule alioripoti jana kwamba walifanya utafiti wakafikia conclusion kwamba lazima zana zipatikane. Nadhani hiyo unaweza ukafikia hiyo hata bila utafiti.

Mheshimiwa Spika, utafiti unaohitajika Mheshimiwa Ulega ni kijana mzuri, msomi mzuri wa Bio-aquatic sciences. Tunachukua Lake Tanganyika, Lake Tanganyika umri wake ni miaka milioni 10, maji ya Ziwa Tanganyika yaliyomo Ziwa Tanganyika ujazo wake ni cubic meter 18,880. Aina ya samaki waliopo ni zaidi ya 350. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Wizara yetu tunataka wafanye utafiti hapa, Ziwa Tanganyika; nikiwa Kigoma nimekaa Kipiri, nimekaa sehemu nyingi huko nafanya utafiti lakini mbona samaki ni aina mbili tatu? Hizi 330 wengine wanaenda kwenye extinction wanapotea sisi bila kuwajua. Tunaenda Ziwa Nyasa, Ziwa Nyasa lina umri wa miaka milioni mbili. Ujazo wa maji kwenye Ziwa Nyasa ni cubic kilometer 8,400, Ziwa Nyasa hilo na lenyewe ndiyo lina samaki wa aina nyingi kuliko aina yoyote hapa duniani. Ni kati ya 800 na 1,000 species of fish. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ripoti zetu hizi species zote 1,000 za Ziwa Nyasa ziko wapi? Tunakuja Ziwa Victoria lenyewe ndilo changa kuzidi yote. Umri wake ni miaka 400,000 lakini ujazo wake wa maji ni cubic kilometer 2,424. Aina ya samaki waliomo Ziwa Victoria ni zaidi ya 500. Kwa hiyo, pendekezo langu la kwanza kwa Wizara yetu hii kwenye haya maziwa makuu matatu yana maji ya kutosha. Yana aina nyingi sana za samaki kama Ziwa Victoria 500. Je, hawa samaki wote wako wapi? Wanavuliwa na nani? Hao wengine.

SPIKA: Mheshimiwa Muhongo kengele ya pili imeshagonga, dakika mbili malizia.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, dakika mbili afadhali. Sasa kwa kumalizia niseme hivi; Ziwa Victoria nimechukua ukubwa wake, Kenya wana 6% ya Ziwa Victoria, Uganda wana 45% na Tanzania tuna 49%. Kenya yenye 6% ina viwanda 18 vya samaki. Uganda yenye 45% wana viwanda 11. Tanzania ambao tuna 49% na ripoti hapa Mheshimiwa Ulega Musoma hatuna kiwanda hata kimoja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo pendekezo langu la mwisho ni kwamba tuwekeze kwenye uvuvi wa vizimba. Tutoe kama hii mikopo iliyokuja nashukuru Mheshimiwa Waziri ameniambia wiki ijayo watu watapewa ile mikopo yao tuvue kwa vizimba lakini vilevile kwa sababu samaki wa vizimba ni wengi tutoe mikopo kwa Watanzania waanzishe viwanda vya samaki kwa sababu samaki wa vizimba watakuwa wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunikaribisha. Wizara ya Kilimo kama ambavyo tumekuwa tunajadili hapa, ina jukumu kubwa sana la kufanya uchumi wetu ukue kwa haraka (accelerated growth) na huko nako mijadala yetu ni kutayarisha Wizara ya Kilimo iweze kutoa mchango wa ukuaji wa uchumi wetu Kitaifa utakaotufikisha asilimia nane mpaka kumi. Kwa hiyo, hii Wizara ina jukumu la kutuhakikishia chakula kipo, ajira inapatikana, ustawi wa jamii na kuongeza pato la Taifa. Wizara inakuja vizuri, kuna mabadiliko, kuna maboresho na ubunifu. Sasa mimi napenda kusisitiza, ameongea Waziri, lakini najaribu kuweka uzito wa mabadiliko na ubunifu anaoufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kilimo chetu kiweze kuwa na tija kubwa, lazima kwanza tuwekeze kwa nguvu zote kwenye kilimo cha umwagiliaji. Sasa kwenye mambo ya umwagiliaji, takwimu hata za kutoka FAO zinaonesha kwamba, mfano mahindi, ukitumia mvua tunayoitegemea kwa hekta moja utavuna karibu tani moja mpaka tani 2.7. Ukienda kwenye umwagiliaji, ni kati ya tani sita mpaka tani tisa. Kule Namibia wameweza kuvuna mpaka tani 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine ni ngano waliyoongea Wizara. Kwa mvua za kudra ya Mwenyezi Mungu, unapata karibu tani nne mpaka tani tano kwa hekta moja, lakini ukitumia kilimo cha umwagiliaji unaenda tani nane mpaka tani 10. Kwa hiyo, maboresho makubwa yaende kwenye umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili ni zana za kilimo (farm implements). Sasa hivi duniani kuna zana nyingi, nitachukua tu tractors. Duniani sasa hivi kuna tractors milioni 16, hatujui Tanzania ziko ngapi, nadhani Wizara itajibu yenyewe. Mfano mzuri wa Tanzania kuiga ni nchi ya India. Mwaka 1961 tukipata uhuru, hekta 1000 India ilikuwa ina tractor 0.19; kwa mwaka 2000 India hiyo hiyo kwa hekta 1000 walikuwa na tractors tisa. Sasa hivi wana tractors 14 kwa hekta 1000. Kwa hiyo, Wizara ya Kilimo ipige mahesabu na yenyewe kwa hekta zetu tunazolima, tuna tractors ngapi? India, ukichukua jimbo linalolima sana la Punjab, wao kwenye hekta 1000 wana tractor 82. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha tatu, ni matumizi ya mbolea ikiwemo samadi. Wataalam wa Kilimo na wakemia wamepiga hesabu, ukichukua tani moja ya mahindi ukalima, ukaivuna, unachotoa ndani ya ardhi, unachopoteza ni kilogramu 25 za Nitrogen, Kilogramu 20 za Potassium, Kilogramu tano za Phosphorus. Kwa hiyo, matumizi ya mbolea ni muhimu sana. Kwa hiyo, katika hekta moja unapaswa kutumia mbolea ili urudishe virutubisho hivyo, unahitaji kilogramu 100 uongeze Nitrogen, kilogramu 100 uongeze potassium oxide na kilogramu 280 uongeze phosphorus pentoxide. Haya ni mambo ya mbolea, yanajulikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha nne ni mbegu bora. Nimemsikia Waziri anaongea vizuri, na hii ni biashara kubwa sana duniani. Sasa hivi biashara ya mbegu inagharimu karibu Dola za Marekani milioni 70. Kwa hiyo, tuwekeze huko. Kwa hiyo, sisi Musoma Vijijini na Mkoa wa Mara kwa ujumla, tunaunga mkono hoja ya bajeti hii kwa sababu tuna mabonde sita Mkoa wa Mara yamewekwa kwenye bajeti, nami Musoma Vijijini nina mabonde mawili; Bonde la Bugwema, Bonde la Suguti Namanyere. Ninachoomba, wale consultants waende haraka tuanze kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusisitiza sasa umuhimu wa kilimo kama biashara kubwa duniani. Mfano ni kwamba, yaani mahitaji ya chakula (Global food demand projections), mwaka 2030 tutahitaji tani bilioni kumi za chakula; na mwaka 2050 tutahitaji tani bilioni 15. Kwa hiyo, kilimo ni biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua mifano ya mazao. Kwanza ni mahindi. Kwa mwaka 2021 wauzaji wakubwa namba moja ni Marekani amefanya biashara ya Shilingi bilioni 18.8 na watatu Ukraine, amefanya biashara ya Shilingi bilioni 5.8. Mwaka 2022, makisio ni kwamba mahindi yatahitajika tani bilioni 1.075. Je, Tanzania tutauza? Kwa sasa hivi, Afrika, wazalishaji na wauzaji wakubwa ni Nigeria, South Africa, Egypt na Ethiopia. Kwa hiyo, Wizara ijitahidi angalau ifukuzane na Nigeria kuzalisha tani karibu milioni 35. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine wa biashara kubwa ya chakula duniani ni mpunga (rice) au mchele ukishakobolewa. Asilimia 50 ya watu duniani ambao sasa hivi ni bilioni nane wanatumia mchele kama chakula kikuu kila siku. Mwaka 2022 biashara ya mchele sasa, umeshakobolewa, thamani yake ilikuwa karibu Shilingi bilioni 300 na wazalishaji wakubwa ni China. Mbali na kuzalisha, lakini bado inanunua kutoka nje. Kilimo chetu, Wizara itusaidie kwenye hekta moja kama hatukupata mavuno mazuri, tuvune tani tatu mpaka sita lakini tukilima kwa uzuri zaidi, tuzidi zaidi ya tani kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara nyingine kubwa duniani ya mazao ni ngano. Kwa sasa hivi tuko watu bilioni nane duniani na bilioni tatu kila siku wanatumia ngano kama chakula. Biashara ya ngano ni kubwa. Mwaka 2020 ilikuwa ya Dola bilioni 155 na inategemewa mwaka 2028 biashara ya ngano itafika Dola bilioni 211. Kwa hiyo, ni busara kubwa sana kwa Wizara kuamua kufufua na kuwekeza kwenye kilimo cha ngano.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wazalishaji wakubwa, lakini mimi nilitaka kuongelea wanunuaji wakubwa, na hapa ndiyo naomba sisi Watanzania tusikilize vizuri. Egypt ananunua karibu Dola bilioni tano kwa mwezi; Nigeria, Indonesia, China na Turkey, Turkey ni karibu Dola bilioni tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Egypt tumewapa miradi hapa, China tumewapa miradi, Uturuki tumewapa miradi, kumbe wananunua ngano. Kwa hiyo, nasi tuwauzie ngano angalau turudishe rudishe kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao lingine ni mihogo. Biashara ya mihogo mwaka 2022 imefika karibu tani milioni 280 na asilimia 70 ya mihogo duniani inazalishwa na nchi tano tu; Nigeria, Brazil, Thailand, Indonesia na Congo. Nigeria inazalisha kwa mwaka tani milioni 60. Sisi tuliomba tupeleke mihogo China hata tani milioni moja hatukupata. Nigeria inazalishwa kwa hekta moja tani 16. Je, kilimo ambacho tunafanya mabadiliko, mihogo tutazalisha kiasi hicho na kuvuka?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wanunuzi wakubwa wa hizi biashara za mihogo, China inatumia Dola bilioni 2.2; Marekani ni ya pili, Dola milioni 150; Japan ni ya tatu Dola milioni 62. Kwa hiyo, ndugu zangu Wizara, wekeni mkazo kwenye kilimo cha mihogo, hata kule Musoma Vijijini nawasubiri kwa sababu wanunuzi wapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nigusia biashara ya maua duniani, yaani yale maua yaliyokatwa yale. Mwaka 2022 hiyo biashara ukubwa wake ulikuwa wa bilioni 36.5. Mwaka 2027 biashara hiyo itafika karibu bilioni 45.5. angalia wazalishaji wakubwa wa maua duniani; suppliers wa kwanza ni Netherlands; wa pili, Columbia; na wa tatu, Ecuador. Sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Profesa, ni kengele ya pili hiyo.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, tena rafiki yangu, nimalizie tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua Kenya ni ya nne. Inauza maua ya milioni 766; Ethiopia ni ya tano, inauza maua milioni 235. Kwa hiyo, nimalizie kwa kusema, hata sisi maua lazima tushindane na Kenya na Ethiopia ili maua yawe ya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, mchango wangu mimi kwanza naunga mkono bajeti, kwa sababu kuna miradi mikubwa ya Musoma Vijijini ambayo inaanza mwezi wa nane, barabara na kilimo cha umwagiliaji na miradi mingi, kwa hiyo, Musoma Vijijini tuunge bajeti hii mkono, ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu mimi utakuwa una takwimu, mjitayarishe kwa takwimu. Ni kwamba ninachangia namna ambavyo uchumi wetu unaweza kukua kwa haraka. Sasa hivi tuko kwenye kati ya 4% na 5%; tulikuwa tuko kwenye 7% tukashuka kwa sababu nyingi zilizoelezwa na kuondoa umaskini hii ni wachumi wa dunia magwiji wote wanasema uchumi ni lazima ukue zaidi ya 8%. Kwa hiyo, kati ya 8% mpaka 10%, ndio mchango wangu mimi; mipango na ukuaji wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulipanga kwenye maendeleo ya miaka mitano ikifika mwaka 2025 tuwe na GDP per capita ya dola 3,000 na kufika huko kwa mahesabu yote wanaojua uchumi, wanaojua mambo ya umeme unahitaji umeme wa megawati 10,000; kwa hiyo, umeme haujatosha.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hali ilivyo ni kwamba GDP per capita yetu mwaka jana ilikuwa dola 1,253; jirani yetu alikuwa GDP per capita dola 2,278; nimechukua Algeria ambayo ina gesi ina GDP per capita dola 4,315; Seychelles naichukua kwa sababu ina elimu bora sana Afrika halafu ndio yenye uchumi bora, ina GDP per capita zaidi ya dola 19,000. Nini tufanye uchumi wetu ukue kwa 8% mpaka 10%?

Mheshimiwa Spika, cha kwanza kabisa ni umeme, alipoishia Dkt. Kalemani, lakini tunahitaji umeme wa uhakika, tunahitaji umeme mwingi na umeme wa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa vipimo vya umeme duniani na hivi ndio vipimo vya kiuchumi, sio kusema unaweza ukafikisha umeme kwenye kijiji, kwenye kitongoji hata ukafikisha vitongoji vyote suala linakuja ni wangapi kwenye hicho kitongoji wanatumia huo umeme. Hicho ndio kipimo cha kiuchumi (electricity consumption power per capita). Vilevile ukifikisha hapo unaweza ukasema wangapi wamepata fursa kwenye hicho kijiji kupata umeme (access to electricity). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba ripoti zetu zinavyotoka Serikalini lazima zitaje hizo takwimu, ukisema tu vijiji na vitongoji hujajibu hoja ya kiuchumi. Sasa angalia mambo ya umaskini na utumiaji wa uchumi. Nimewatajia Seychelles GDP per capita yao zaidi ya dola 19,000; power per capita ni units 4,514 tunaiita sisi unit, lakini ni kilowatt hour. Unakuja Algeria yenye gesi, umeme wanaotumia power per capita ni units 1,600; unachukua Kenya ambayo inatuzidi GDP per capita, power per capita yao ni unit 170 na Tanzania ni 103, hizi ni kidogo ni chache kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Tanzania tufanyeje? Cha kwanza tuongeze umeme na vyanzo vya umeme viwe vingi, siyo kimoja. Tatizo letu ukisema vyanzo vingi wengine wanasema unachukia bwawa, ni watu wasiokuwa na uelewa. Tunataka vyanzo vingi na umeme wetu utokane na natural gas, utokane na maji, utokane na makaa ya mawe. Halafu unaenda kwenye renewables yaani geothermal, solar, wind, biomass, biogas, tides and waves. Hapo lengo letu ni kufikisha umeme wa megawati 10,000. Hapo ndio tutaanza kusema sasa uchumi unaanza kukwamuka.

Mheshimiwa Spika, bei ya umeme nayo napendekeza ipunguzwe, sasa hivi umeme majumbani ni US cents 9.7 kwa unit, viwandani ni unit 10 ndio zinatumika US cents 10 kwa unit. Kenya wako juu, lakini hii siyo sababu ya kufanya sisi tusipunguze umeme kwa sababu eti nchi za Afrika Mashariki umeme bei iko juu. Kwa hiyo, bei ikiwa chini watumiaji watakuwa wengi. Sasa ili uchumi ukue kwa kasi tunahitaji umeme mwingi na tufikishe zaidi ya megawati 10,000.

Mheshimiwa Spika, kingine cha pili ambacho kitafanya uchumi ukue kwa kasi na umaskini uzidi kutokomea, tuna mambo ya kilimo sawa, mambo ya madini sawa, mambo ya utalii sawa. Kuna kimoja ambacho lazima bajeti inayokuja iwekee mkazo ni uchumi wa gesi. Uchumi wa gesi ni hivi, natoa Algeria ndio ina-export LNG ya kwanza Afrika nzima, ina-export tani 29.3 kwa mwaka. GDP yake niliyowatajia zaidi ya dola 3,000. Qatar ndio ina-export LNG ya kwanza duniani ni tani 80,000,000. GDP per capita ya Qatar ni zaidi ya dola 84,000.

Mheshimiwa Spika, sasa Tanzania tufanyeje? Lazima tuongeze mambo ya gesi. Sasa hivi tunazo hizo trilioni 57.5 ni nyingi, lakini hatujafanya kazi zaidi. Algeria wanazo 159 TCF, Mozambique majirani zetu wanazo 100 mpaka 200 TCF. Kwa hiyo, Tanzania tufanye nini? Lazima tutafute mafuta na gesi kwa bidii zaidi na ndiyo maana mimi mpaka leo hii naamini kabisa kwamba TPDC haifai kufanya kazi ya kuuza mafuta ambayo inaweza kufanywa na kila mtu. Lakini kila mtu hawezi kutafuta mafuta na gesi.

Mheshimiwa Spika, Mozambique wanaanza ku–export LNG kwa gesi inayotoka Ruvuma Basin. Sasa sisi tuko na wao kwenye Ruvuma Basin. Tunapaswa kuiuliza TPDC huko tuna gesi kiasi gani? Tuna mafuta kiasi gani? Maana yake wenzetu kwenye hiyo basin wameshapata over hundred trillion cubic feet of natural of gas. Sisi huku chini hatujafanya explorations. TPDC iende huko, iache kuuza mafuta. Hatujatafuta mafuta kwenye Ziwa Tanganyika, kwenye Ziwa Nyasa, kwenye Ziwa Rukwa na muhimu zaidi tena wewe Spika ni mwanasheria, huko tunakoenda kuna hizi resources zitakuwa kwenye mipaka ya nchi mbili, kwa hiyo, TPDC ina kazi mafuta na gesi yakipataikana Ziwa Tanganyika, sisi na Congo na Zambia mambo yatakuwaje? Tukienda Ruvuma Basin tukapata gesi na Mozambique wana gesi hiyo shared resource itakuwaje?

Kwa hiyo, tuweke mkazo kwenye utafutaji wa gesi na mafuta na wataalamu wapo tumewasomesha ambao mimi nawafahamu tumewasomesha Norway tulipeleka Masters 40, hatujui wanafanya kazi gani? China tulipeleka Masters Ph.D 100, vijana wengi wamesoma kwenye oil and gas hawana kazi.

Sasa natural gas; uchumi wa gesi kwa Tanzania matumizi ya kufanya uchumi ukue cha kwanza kabisa tuzalishe umeme yaani kilowatt hour moja hiyo unit moja inahitaji cubic feet 7.36 kuzalisha unit moja ya umeme na sisi tuna materials na uzuri wa umeme na gesi hauna ukame, hauko capital intensive. Kwa hiyo, umeme mwingi tungeutoa siyo kwamba tunasimamisha maji, lakini tungewekeza sana kwenye gesi tupate umeme mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha pili, uchumi wetu kukua kutokana na natural gas.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia Profesa.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Spika, ni mambo ya mbolea na mambo ya viwandani.

Sasa nimalizie hiyo dakika moja kwa biashara ya LNG. Biashara ya LNG itatusaidia kwa sababu duniani sasa hivi kufika mwaka 2030 biashara hiyo itakuwa na ukubwa wa dola bilioni 210; Tanzania lazima ipate pale. Msumbiji wana LNG plants mbili, ya kwanza inaitwa Floating LNG ambayo gesi wameenda kuichukua huko huko baharini na wameanza kusafirisha tani 13,000,000 kwa mwaka za LNG na nyingine wanayoitengeneza wataanza na tani 12,800,000 lakini wataenda mpaka milioni 43,200,000. Kwa hiyo Tanzania kama tunataka uchumi wetu ukue kwa haraka ni lazima tuwekeze kwenye umeme, tuzalishe uwe mwingi, halafu lazima twende kwenye uchumi wa gesi na huu uchumi una vitu vingi sana na ushauri mwingine ni kwamba kwa sababu kuna viwanda vingi kama hivi nimewaambia umeme, mbolea na viwandani kabla haujampatia mshindani wako gesi yako, nadhani ni busara umpatie bidhaa zinazotokana na gesi kuliko kumpatia gesi yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia muda. Napenda kutoa ushauri kwa TANROADS, swali la kwanza la kujiuliza kwa TANROADS ni kwa nini miradi yote ya Mikoani imekwama? Mimi nadhani kimoja ni kwamba miradi ninavyoelewa TANROADS kuna miradi inasimamiwa na Mikoa na kuna miradi inasimamiwa na Makao Makuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda muda umefika wa TANROADS watafakari zaidi kwanini wasiwe TANROADS moja, miradi inasimamiwa toka Makao Makuu, mikataba inawekwa toka Makao Makuu na wengine wanafuatilia, huo ndiyo ushauri wangu wa kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wa pili kwa TANROADS ni kweli kwamba Wabunge tunafurahia lakini barabara yangu yenye kilometa 92 kwa wastani inachukua mwaka mzima kutayarisha barabara kabla ya kuweka lami, kwa hiyo, itachukua miaka siyo chini ya Ishirini, hii barabara haitakamilika!

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti nimepitia randama nzima wastani ni Shilingi Bilioni Moja na Bilioni Tatu, ni fedha zinaonekana ni nyingi lakini kiujenzi ni fedha kidogo sana. Sasa TANROADS inabidi vilevile wajiulize je, kuna ufanisi mkubwa wa kutoa fedha kidogokidogo barabara ichukue miaka Ishirini, Hamsini kujengwa au itakuwa Serikali inaingia hasara kwasababu kila ikijenga baada ya muda fulani inarudi tena kurekebisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine kwa TANROADS ni kwamba wajaribu kufuatilia ujenzi wa barabara umeenda unabadilika, nilikuwa na mtaalam mmoja amegundua njia nzuri sana ya kujenga barabara za kisasa kuachana na hizi tulizozizoea tunazoziona za TANROADS. Kwa hiyo, huo ndiyo ulikuwa ushauri wangu upande huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikija barabara yangu ambayo kiuchumi ni muhimu kwelikweli inapita pembezoni mwa Ziwa Victoria, tunazo samaki, tunayo madini, tunayo pamba, alizeti, barabara hii kama nilivyokueleza huenda itachukua miaka 50 kukamilika. Kwa hiyo, nimejadili na Waziri kwa muda mrefu na mimi kawaida yangu huwa sipendi kuongea ambayo nimejadili na wataalam isipokuwa Mkandarasi lazima wamwangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija upande wa Wakandarasi ukweli ni kwamba tunawapenda wazawa lakini napenda kutoa pendekezo TANROADS, Wakandarasi wote wanaochelewesha miradi awe ni mzawa awe ni Mkandarasi wa kutoka nje, lazima muwe na mikakati mipya. Mkakati wa kwanza muweke kwamba kama mtu hakamilishi mradi kwa muda akichelewesha sidhani kwamba huyo anastahili kupewa mradi mwingine tena. Inavyoonekana ukisikiliza Waheshimiwa Wabunge wote hapa kilio chetu kinafanana, Wakandarasi hawamalizi kwa muda Wakandarasi hawalipwi kwa muda, sasa hii bodi inayo register ma-Engineer ni lazima ianze kuwa na orodha ya blacklist yaani Wakandarasi ambao hawawezi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho naomba TANROADS wawekee maanani ni pale wanapompatia Mkandarasi ambaye tayari ana madeni, kama wa kwangu nilifuatilia kwelikweli ndiyo maana nikakaa kimya nikajua huyu hata miaka Mia Moja hatamaliza kwa sababu zile fedha zangu anazolipwa kujenga barabara yangu ya lami ndiyo anaenda kulipia madeni yake ambayo hayanihusu mimi kabisa, nadhani Waheshimiwa Wabunge hali ndiyo hiyo hiyo. Mkandarasi yupo Mkoa ‘X’ anapewa kazi mkoa Y, akipata fedha za Mkoa ‘Y’ anaenda kulipia deni la Mkoa ‘X’. Kwa hiyo, tutumie ile Sheria ya Mfilisi mtu akiwa amefilisika haaminiki na huwezi ukampatia kazi. Kwa hiyo, naomba TANROADS wasitoe kazi kwa makampuni ambayo mienendo yao kifedha ni mibovu na wengine wanakuwa wamefilisika, wanatupatia matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine tena ambacho TANROADS wajiulize je, hizi penalties ambazo wanazipiga hawa Wakandarasi waliochelewesha mbona hawagutuki wa hawastuki hawafanyi chochote? Ina maanisha kwamba hawaogopi wala hawachukui kitu serious kutokana na hiyo penalties ambazo wanapigwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija upande wa kivuko nadhani dakika zangu bado zipo. Ninacho Kisiwa kimoja kinaitwa Rukuba hiki kisiwa ni mashuhuri, kina wavuvi wengi na watu karibu wa East Africa wapo kwenye hiki Kisiwa nimeomba kivuko kwa muda sasa nadhani leo Mheshimiwa Professor atakiwekea maanani, kinaitwa Kisiwa cha Rukuba ninashukuru Serikali na ninamshukuru na Mheshimiwa Rais alishatoa Milioni 250 wameanza kujenga Kituo cha Afya, juzi nilikuwa tena Jimboni wamepewa tena Milioni 250 kwa hiyo zimefika 500 nadhani Serikali bado itaongeza fedha Zaidi, lakini Kisiwa kinahitaji kivuko na hiki kivuko naomba kiunganishe wilaya mbili ambazo ni Wilaya ya Rorya kwenye Kijiji cha Kibui halafu na Wilaya yangu lakini kitatoka Rorya kinapita kwenye hiki kisiwa halafu kinakuja hapa Musoma Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hicho kivuko hakipo kwenye bajeti ya mwaka huu lakini nakiomba kwenye bajeti ya mwaka ujao. Kivuko kingine cha muhimu cha kufanyia marekebisho, kivuko ambacho kinaunganisha Wilaya ya Bunda na Wilaya yangu ya Musoma. Kule Bunda inatokea Mwibara Kijiji kinaitwa Iramba. Sasa kile kivuko kuja huku kwangu Kurugee ni cha siku nyingi walichukua kivuko chakavu kutoka Mwanza wakaona watusaidie, kweli walitusaidia lakini ni kibovu. Kwa hiyo, tunaomba kivuko kipya kile ni chakavu, tulikitumia kwa muda tukiwa na mategemeo kwamba kivuko kipya kinaletwa cha kutoka Iramba kuja Kurugee. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Profesa kwa mchango wako.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: …fedha tupitishe tupewe vivuko vipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Wabunge tupitishe hii bajeti kwa sababu mimi vitongoji vyangu 374 tayari nimeshavipeleka REA na Januari nazunguka navyo kama unavyo nitakutumia tu sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya kusema hayo naomba mchango wangu uwe wa picha kidogo usiwe wa jimbo tu. Ni kwamba wakati tulitengeneza plan yetu ya miaka mitano tukawa tunasema tutaishia 2025 ilikuwa hivi; GDP per capita yetu lengo letu lilikuwa kufikia dola 3,000 na kufikia hapo tulikuwa na mipango au tunayo mipango ya umeme jumla installed capacity kuwa megawatt 10,000 mpaka megawatt 15,000 na ndugu zangu Wabunge nawaomba niwaeleze ukitaka uchumi ukue kwa zaidi ya asilimia nane kwenda asilimia kumi, unahitaji umeme mwingi na wa bei nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya sasa ya senti 11 kwa unit bado ni umeme wa bei ghali. Sasa tulivyosema kama tukishindwa kufikia megawatt 10,000 mpaka 15,000, wakati tukiwa GDP per capital ya Dola 1,500 yaani nusu yake, tunapaswa kuwa na umeme installed capacity ya megawatt 5,000. Ndiyo maana ukiangalia kwenye document za Serikali zimewekwa kwamba kufikia mwaka 2025 tunapaswa kuwa na megawatt 5,000. Kwa hiyo, niwakumbushe tu kuwa na megawatt hizo ni lazima tuwe na vyanzo vingi, tujadili kila vyanzo lakini tusing’ang’anie kimoja, viwili bado hatutafikisha megawatt 5,000. Lengo letu ni megawatt 5,000 ifikapo 2025. Kwa hiyo, bado ndiyo maana nasema tupitishe hii bajeti ili kusudi tufike huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa upande wa umeme na maendeleo lazima ujilinganishe na ushauri wangu kwa Wizara nimeshawapatia Vitongoji 374, lakini mimi kuangalia maendeleo ya upatikanaji wa umeme nchini sitahesabu Vitongoji wala Vijiji, nitachukua hesabu ambazo zinatumika Kimataifa. Sasa Kimataifa unachukua unit ambayo Wizara inapaswa kutuambia ni energy per capital, yaani tukitupia vyanzo vyetu vyote tukagawa na population ya Milioni 62, je kila mtu ana unit ngapi, hizo ndizo zinahitajika. Lakini nzuri zaidi Vitongoji nimewapa nitakachoenda kuangalia mimi je, watu wa Kitongoji ‘X’ ni wangapi wanatumia umeme, ndiyo kipimo muhimu sana. Kwa hiyo, kwenye ripoti ya Wizara ninaomba mtoe ripoti ya energy per capital halafu mtoe electricity energy consumption per capital. Ukichukua hivyo vipimo unakuta kwamba Kenya, IMF inasema mwaka 2002 GDP per capital ya Kenya itakuwa Dola 2,252 na ya kwetu ni Dola 1,260.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wenye GDP per capital ya dola 1,260 Tanzania, installed capacity yetu ambayo imeandikwa Kimataifa na hiyo huwezi ukaidanganya kwa sababu unavyonunua turbines duniani wanaweka kwenye database, kwa hiyo wanajua nchi fulani wana uwezo wa kuzalisha umeme kiasi fulani. Kwa hiyo, installed capacity yetu ambayo iko reported Internationally ni megawatt 1,605.86. GDP per capital ya Kenya ambayo ni 2,252 wanazo megawatt 2,840, kwa hiyo lazima tushindane na Kenya kwa sababu alivyokuwa anaeleza Waziri transmission lines tulizozijenga za 400KV kupita Namanga na 400KV kwenda Zambia nia kubwa ni kununua umeme na kuuza umeme ndiyo uchumi wa kisasa duniani kote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ili tuweze kuwa na umeme mwingi tuendelee na hii miradi, energy mix yetu Tanzania ambayo ipo kwenye vitabu vyetu tumesema tutazalisha umeme kutokana na natural gas ya kwanza, pili itakuwa hydro, tatu itakuwa ni coal na nne itakuwa ni renewable energies. Sasa renewable energies zipo zaidi ya 11 lakini wengi wanajua solar na wind, lakini zipo 11 hiyo nayo kuna siku nyingine tutajaribu kuijadili. Lakini ukilinganisha na Kenya sasa, maana yake Kenya waliwahi kutuomba tuwauzie megawatt 1,000 ya umeme walivyokuwa wanaona miradi yetu inaenda kasi lakini sasa unaona wanatuzidi. Kwa hiyo sidhani kwamba wanategemea sisi tuwauzie umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia Kenya wanavyofanya vizuri, kwenye geothermal wanazo megawatt 863, ndiyo wanaongoza Afrika kwa kuwa na megawatt 863, halafu Waheshimiwa Wabunge mmesikiliza michango humu matatizo ya ku-develop geothermal siyo kwamba yako Wizara ya Nishati havihusiani kabisa, completely outside the scope of the problems of geothermal energy development in the country, completely out. Kenye wind wanazo megawatt 437 linganisha na Tanzania, solar wana megawatt 173 sasa hizi nazitaja kwa sababu Tanzania tupo kwenye East African Power Pool, lazima tuuziane umeme. Halafu tuko kwenye SADC Power Pool kwa hiyo nadhani Mheshimiwa Waziri Wizara yako inavyotoa ripoti nzuri za Kitaifa lazima zionyeshe hali ya umeme ndani ya East Africa na ndani ya SADC kwa sababu sisi tunanunua umeme Uganda, sisi tunanunua umeme Zambia, sisi tunanunua umeme Kenya ndiyo maana tumejenga transmission lines tuzalishe umeme mwingi na sisi tuanze kuuza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikiacha suala la umeme kwa ajili ya muda ninakuja kugusa kidogo kwenye mambo ya oil and gas. Muda usiponiruhusu nadhani nitaongea kwenye bajeti ile ya fedha kuhusu uchumi na gas. Kwenye oil and gas upande wa TPDC ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge ushauri wangu ni TPDC ambayo ilianzishwa mwaka 1969 iachwe na majukumu yake. Haya ya biashara ya mafuta kwa sababu waliopo pale TPDC ni Ma-geologist, Ma-geophysics, Seismologists, Geochemists wewe unawapeleka kwenye biashara ya mafuta haviendani na siyo eneo lao hilo! Kwa sababu TPDC bado kazi wanayoifanya hawajaifanya hata kwa asilimia 20. Wewe muulize TPDC inapaswa kutueleza Je, Tanzania kuna mafuta? ndiyo maswali tunauliza TPDC! Siyo kuuliza TPDC mafuta kwenye petrol stations za MOIL hapana! (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapaswa kuiuliza TPDC Je, Tanzania tunayo gas kiasi gani? Kwa mfano, sasa hivi Tanzania ni nchi ya 10, unajua wengi wanaongea tunayo gas nyingi, sisi ni wa 10 kwenye reserves kwa Afrika kwa dunia itakuwa kwenye mamia naongelea Afrika. Kwa hiyo ukiangalia Afrika ya kwanza Nigeria ina TCF 209, Algeria 159, Senegal 120, jirani yetu Msumbiji ana ripoti 100, lakini ambayo wanayo hawajaripoti wako kwenye 200. Ndiyo maana TPDC mimi sitaki iingie kwenye mambo ya kununua na kuuza mafuta kwa sababu hii gas 200 TCF za Msumbiji wamezipata Province ya Capo Delgado, ni kwenye Ruvuma basin. Sisi Ruvuma basin hatujaanza kufanya exploration, utaitoaje TPDC kwenye exploration na huko Kusini ndiyo tunayo gas nyingi kuacha hii tuliyonayo. Kwa hiyo, pendekezo langu mimi ni kwamba TPDC iwezeshwe na lakini siyo kununua na kuuza mafuta, iwezeshwe kufanya exploration. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna hii nafasi iliyopatikana vita ikipiganwa duniani, European Union asilimia 40 ya gas yake inanunua kutoka Russia, hizo ni 155 billion Cubic metric tons, 40 percent. European Union imezunguka nchi za Kiafrika kujaribu kununua gas lakini haijaja Tanzania kwa sababu sisi bado! Ndiyo maana TPDC waachwe kwenye core mission yao ya oil and gas exploration and development. Hata lile jina lenyewe jamani TPDC, Tanzania Petroleum Development Cooperation, haliitwi Tanzania Development Trade, unaona ile ‘T’, unaona tofauti hapo? Kwa hiyo tuwaache TPDC huko. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Mengine nitaongea siku nyingine. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuongea. Nianze kwanza kwa kusema kwamba bajeti tuliyopewa ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, ni bajeti nzuri, na mimi kwa Jimbo la Musoma Vijijini miradi yote tuliyoiomba imekubaliwa. Kwa hiyo, hii bajeti naiunga mkono kwa niaba ya wananchi wa Musoma Vijijiji. Kwa hiyo kinachofuata ni namna ya kuboresha au kudumisha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitachukua picha kubwa zaidi kwa sababu Jimbo limeshapata kila kitu, sasa nifanye kitu cha kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo. Mheshimiwa Waziri amefanya presentation nzuri sana na akatuonesha hali ya uchumi ilivyo duniani. Nitaongezea tu kwamba, kwa hali tuliyonayo ya uchumi sasa hivi, wataalam wabobezi wa uchumi duniani wanasema ni hali kama ilivyokuwa mwaka 1973 na 1974 ambapo mafuta yalipanda bei mara nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1979 na 1980 mafuta yalipanda bei mara mbili, na watu wa umri wangu wanakumbuka hii ya pili ya mwaka 1980 ndiyo mapinduzi yaliyomtoa Shah, kwa hiyo, Iran haikutoa mafuta vilivyo. Kwa hiyo, mwaka 1973/1974 tulikuwa na hali ngumu, mwaka 1979/1980 tulikuwa na hali ngumu, lakini Mheshimiwa Rais wa wakati huo, Baba wa Taifa aliweza kutuvusha. Nami nina imani kwa hali tuliyonayo sasa hivi, Rais wetu Mheshimiwa atatuvusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nampa pongezi nyingi sana kwa bidii anayoifanya. Uchumi wa sasa hivi wana neno la Kiingereza linaitwa Stagflation. Stagflation ni uchumi ambao uwekezaji unapungua, investments hazipo. Ndiyo hali tuliyonayo sasa hivi duniani na Watanzania tuko hapo hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndugu zangu tutatokaje hapo kwenda mbele? Mimi nachukua mambo tuliyokuwa tumekubalina kwenye Dira yetu ya Maendeleo na Mipango ya Miaka Mitano. GDP per capital yetu kwa sasa ni Dola 1,260, tunataka tufike GDP per capital Dola 3,000 mwaka 2025. Mwaka 2025 tutakuwa Watanzania karibu asilimia 70.1. Kwa hiyo, tunachokifanya ni kwamba GDP yetu sasa hivi ambayo ni ya Dola za Marekani 62 billion, tukichukua GDP per capital ya Dola 3,000 kwa kila mmoja, kwa hiyo, mwaka 2025 tunapaswa kuwa na GDP ya Dola bilioni 210. Angalieni kazi hiyo, kutoka Dola bilioni 62 kwenda Dola bilioni 210.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo hapa nakuja kutoa ushauri. Umasikini kwa mwaka 2020, poverty rate ilikuwa asilimia 27.1 na mwaka jana 2021 imepungua ikafika asilimia 27. Kwa hiyo, speed ya kupunguza umasikini bado iko chini na inaendana na uchumi. (Makofi)

Mheshimia Mwenyekiti, matumizi ya umeme nadhani niliwahi kuwaeleza kwamba kipimo kizuri kinachotumika Kimataifa siyo kwamba umeme umefika kijijini, umeme umefika kwenye Kata, umeme umefika sijui wapi? Swali watu wanalotaka kujibiwa, ni watu wangapi kwenye eneo hilo wanatumia umeme; na ni umeme kiasi gani? Sasa records ambazo ziko huko duniani zinaonesha hivi, sisi electricity energy consumption per capital Tanzania ni Kilowatt 95. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jirani yetu Kenya ni Kilowatt 170. Sasa Kilowatt 95 yaani ni umeme ambao unaweza ukautumia ndani ya saa moja, ndiyo kipimo cha Kilowatt hour. Kwa hiyo, sisi ni Kilowatt 95, Kenya ni Kilowatt 170. Ndiyo maana wakati ule nilijadili mambo ya energy mix na leo nimesikia Wabunge wengine wamesema wanataka umeme wa upepo na umeme wa jua.

Mheshimiwa Mwenyekiti na ndugu zangu, tukitaka kufanikiwa kwenye mambo ya umeme, lazima twende kwenye umeme wa jua na umeme wa upepo. Kwa mfano, kwa umeme wa jua, China wana Gigawatt 252. Yaani Megawatts 2,250; kwenye upepo wana Megawatt 281,000. Kwa hiyo, kuendana na uchumi wetu ili tuongeze power per capital, lazima tuzalishe umeme mwingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kazi tuliyonayo na Mheshimiwa Waziri aliieleza vizuri, uchumi ulishuka ukaja 4.9 percent, mwakani unataka kwenda 5.3 percent, lakini kupunguza umasikini lazima uchumi uende kati ya percent nane na kumi. Tutafikaje huko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la kwanza, kwa ajili ya muda sitaingia ndani, na ndiyo maana nataka mje mwangalie percent ninazoziweka mimi. Growth; kilimo, uvuvi na ufugaji, tuwekeze pale na itatoa ajira mpya na tuseme growth yake iwe kati ya percent moja na mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili, tuwekeze kwenye utalii ambayo tunaheshimu mama amefanya film ambayo ina-promote utalii, iwe percent moja. Tatu, ni madini. Twende kwenye gold na msisahau gold reserve, nilishaiongelea gold reserve; tuweke kwenye gemstones, tuweke kwenye critical technical metals, technology metals; hili nalo nilishawaeleza na tutumie gesi yetu ya Helium. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, madini yachangie growth ya 3.4 percent halafu tuuze umeme. Cha muhimu sasa ambacho nataka nikiongee, leo nilitoa ahadi, ni uchumi wa gesi. Uchumi wa gesi unaweza ukachangia growth ya five to six percent. Nini maana ya uchumi wa gesi? Gesi ina uchumi mzuri kwa sababu mbili; kwa sababu gesi unaweza kuitumia kama malighafi, halafu gesi unaweza ukaitumia kama source of heat. Ni vitu viwili vinafanya gesi inakuwa muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uchumi wa gesi; kwa hiyo, gesi asilia tutatengeneza mbolea, tutazalisha umeme, kutakuwa na plastics na fabrics, hii SNG waliyokuwa wanaongea ya kwenye magari; tutakuwa na kemikali kama LPG, gesi mnayotumia kupikia, ammonia ambayo iko kwenye mbolea na kwenye ma-refrigeration; methanol ambayo inatumika kwenye plastics, ascetic acid ambayo inatumika kwenye kutunzia vyakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali linakuja: Je, hiyo gesi tunayo ya kutosha? Kuzalisha umeme unahitaji thousand cubic feet kuzalisha one Kilowatt Hour. Unahitaji seven thousand cubic feet kuzalisha one megawatt hour. Je, hiyo gesi tunayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, mbolea. Unahitaji 0.57 tons of ammonia ku-produce one ton of urea. Tatu, unahitaji 33 metric million British thermal unit ya natural gas ku-produce one ton of ammonia. Nne, tunaenda vizuri Serikali, mkataba wa awali umewekwa, bei ya LNG tungekuwanayo sasa hivi, Januari mwaka jana 2021 ilikuwa US Dollar sita kwa 1MMBTU (Metric Million British Thermal Unit).

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Waheshimiwa kuna simu inalia mpaka huku tunasikia jamani. Naomba mpunguze au mzime.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitunzie muda wangu nami nimesimama.

MWENYEKITI: Mheshimiwa kengele ilikuwa imeshalia na huku simu zinalia.

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa, naomba basi nimalizie hizo dakika mbili. Kwa hiyo, sasa hii gesi ndiyo maana napendekeza TPDC ibaki kwenye kazi hii, kwa sababu sasa hivi tumeshagundua 57.54 TCF. Jirani yetu Mozambique ambaye yuko kwenye Ruvuma Basin ameshagundua a hundred TCF na huenda ana two hundred. Kwa hiyo, TPDC isipoweka mkazo huko Ruvuma, tutajua tuna gesi kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni conventional, kuna aina nyingine ya gesi inaitwa shell gas. Hii shell gas ni nyingi sana, ndiyo Marekani inatumia sasa hivi, wala hatujawahi kuanza exploration. Lake Tanganyika inabidi TPDC ieleze kuna mafuta au gesi? Halafu lazima tujadiliane na Kongo na Zambia. Lake Nyasa kuna mafuta na gesi, lazima tujadiliane na Malawi. Halafu kwenye Lake Eyasi na huku baharini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, ndiyo maana mapendekezo yangu nasema kwamba TPDC wana kazi kubwa, kubwa, kubwa, tuwaache watutafutie hii gesi kwa ajili ya uchumi wetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Prof. Sospeter Muhongo. (Makofi)

MHE. PROF. SOSPETER M. MUHONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, ahsante. Mengine nitaongea siku nyingine tena. Ahsanteni. (Makofi)