Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Sikudhani Yasini Chikambo (18 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kuwepo katika Bunge hili. Haikuwa rahisi lakini kwa uwezo wake leo niko hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati ya moyo wangu napenda sana niwashukuru wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kwa kuendelea kukiamini Chama cha Mapinduzi, kwa kuchagua kwa kura nyingi viongozi wanaotokana na CCM. Wamempa kura nyingi Mheshimiwa Rais, lakini wamechagua Wabunge wote wanaotokana na CCM, nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niahidi mbele yako kwamba nitashirikiana na Wabunge wa Mkoa wa Ruvuma wanaotokana na CCM nikiamini kwamba wao wamechangia uwepo wangu katika Bunge hili. Ninaahidi kufanya nao kazi hasa zinazohusu akina mama usiku na mchana. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kabla sijaendelea kusema niunge mkono hoja, lakini nianze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Naomba nipongeze sana hotuba hii imekaa vizuri lakini kwa kuwa ni wajibu wetu kusema neno na mimi naomba niseme neno.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la shilingi milioni 50 za kila kijiji. Sote tunafahamu kwamba Mheshimiwa Rais wetu alitoa ahadi kwa wananchi wetu kwamba Mwenyenzi Mungu akimjalia kushinda katika nafasi hii…
MHE. ZUBEDA H. SAKURU: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sikudhani, naomba ukae.
KUHUSU UTARATIBU......
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimwambie kwamba miongoni mwa mabingwa wasemaji bila kusoma ni pamoja na mimi. Naomba nimhakikishie hilo na ili kuthibitisha naomba niendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuzungumzia shilingi milioni 50 ambazo Mheshimiwa Rais alitoa ahadi kwa wananchi wetu. Namuomba awe anaangalia ahakiki kama hapa nilipo sisomi ili kumthibitishia kwamba niko vizuri na sina shaka, nimepikwa nikapikika. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu wakati anaomba kura alitoa ahadi ya kutoa shilingi milioni 50 kila kijiji na mimi napongeza ahadi hii na sina shaka ahadi itatekelezwa na kwa bahati nzuri kwenye hotuba ya Waziri Mkuu imeelezwa. Kwa kuwa zoezi hili la ugawaji wa hizi pesa wamesema watahakikisha zinatolewa kupitia SACCOS na baada ya utaratibu huu kukamilika kinachofuata sasa ni utekelezaji. Nashauri kabla hatujafika kwenye hatua ya utekelezaji maelekezo yatolewe kwa wananchi wetu ya namna njema ya upatikanaji wa pesa hizi ili kusitokee mkanganyiko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo mbele ya Bunge lako kwa sababu hivi tulivyo hapa kule vijijini tayari akina mama wanaendelea kuchangishana pesa na kufungua akaunti. Inawezekana kabisa wakafungua akaunti lakini mwishoni mtu akajikuta hapati kile alichokusudia. Kwa hiyo, naomba yatolewe maelekezo wakati tunaingia kwenye utaratibu huo kila mmoja anajua vigezo gani vitatumika vya kutoa hizi pesa. Sina shaka na Serikali yangu, naamini watatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu amezungumzia pia masuala ya Mfuko ule wa TASAF. Mheshimiwa Waziri Mkuu atakubaliana na mimi kwamba jambo hili ni jema na kwa kweli linasaidia kaya maskini na kwa bahati nzuri wameelezea kaya ambazo zimenufaika na kiasi ambacho kimetolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama vile ambavyo tunahakiki watumishi hewa, naomba na katika eneo hili turudi tuhakiki wanufaika. Kwenye eneo hili kuna watu ambao wananufaika lakini siyo maskini kama vile ambavyo tumekusudia. Kwa hiyo, inawezekana kabisa jambo likawa jema lakini lisilete manufaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Ofisi ya Waziri Mkuu kama vile ambavyo tunahakiki watumishi hewa basi na kwa upande wa TASAF kwa kuwa tumekusudia kusaidia kaya maskini, twende tusaidie kaya maskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la ugawaji wa maeneo ya utawala. Kama nilivyosema kwamba mimi natokea Mkoa wa Ruvuma lakini naomba niizungumzie Wilaya ya Tunduru. Wilaya ya Tunduru ni miongoni mwa Wilaya kongwe katika nchi hii, ina Kata 39 na Majimbo mawili. Tumezungumza kwenye vikao vyetu na tumeomba kupata Wilaya nyingine. Niombe kupitia ofisi yake wakati utakapofika basi waiangalie na Wilaya ya Tunduru kwa kuiweka katika mgawanyo ule wa kuongeza Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nafikiri huwa tunaongeza maeneo ya utawala kwa ajili ya kurahisisha kutoa huduma kwa wananchi wetu. Kwa dhati ya moyo wangu na kwa bahati nzuri Waziri Mkuu ni msikivu na naamini pale alipo Waziri Mkuu ananisikia, wakati utakapofika wataangalia na kuipa umuhimu Wilaya ya Tunduru. Wala hapigi story Mheshimiwa Waziri Mkuu pale ananisikiliza. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la asilimia 10 ya mikopo ya wanawake na vijana. Kwenye eneo hili wachangiaji wamesema kwamba utaratibu wa siku za nyuma tulikuwa tunaziagiza Halmashauri zetu zitenge asilimia 10 kwa ajili ya kusaidia mikopo ya wanawake na vijana. Mimi naomba ukubaliane na mimi kwamba yako maeneo hayafanyi vizuri. Naomba sana sana tusisitize Halmashauri zetu zitenge hizi pesa kwa ajili ya kusaidia wanawake na vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yako mengi ya kusema lakini naomba niseme mimi ni mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Masuala ya UKIMWI. Wewe utakuwa shahidi, Kamati ya UKIMWI imewasilisha taarifa yake hapa, miongoni mwa mambo ambayo tumekuwa tukiyajadili kwenye vikao vyetu ni kwamba utaratibu wa uendeshaji wa Bunge hauna tofauti sana na utaratibu wa uendeshaji wa Halmashauri. Utakubaliana na mimi kwenye Halmashauri zetu Kamati hizi haziko kama zilivyo kwenye Bunge. Tulileta maombi kwako, tulikaa na wewe, nikubali inawezekana kabisa kabla sijawa Mjumbe wa Kamati pengine nilikuwa sijajua ugumu na tatizo kubwa lililopo la dawa za kulevya na UKIMWI lakini nilipokuja kwenye Kamati hii nimeona kwamba hili tatizo ni kubwa na Wajumbe wenzangu watakubaliana na mimi kwamba ni tatizo kubwa. Tumewasilisha hapa bajeti yetu, tutaomba Bunge liridhie kwa kile ambacho tumeomba na wakati utakapofika basi kitolewe kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunaomba kwa heshima na unyenyekevu na tunaamini nyie viongozi mlioko mbele ni sisi ndiyo ambao tumewaweka na kiongozi msikivu ni yule anayesikia kilio cha watu anaowaongoza, tunaomba sana Kamati hii irudi kwenye mfumo uliokuwepo huko nyuma ambapo Wajumbe wa Kamati hii walikuwa wanapata nafasi ya kushiriki kwenye Kamati nyingine. Wanakuwa na nafasi ya kwenda kuzungumzia masuala ya barabara, maji, zahanati lakini leo sehemu kubwa sisi ni ku-deal na masuala ya maboksi ya condom, masuala ya dawa za kulevya na uingizaji wa vidonge hivi vinavyowasaidia wenye UKIMWI. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikuombe kwamba katika eneo hili, naamini wewe ni msikivu na Spika ni msikivu na wote nyie ni wasikivu na mmekaa hapo kwa ajili ya kusikiliza kilio cha watu mnaowaongoza na sio wengine ni pamoja na sisi Wajumbe wa Kamati hii, tuko tayari kufanya kazi. Kwa nafasi hii naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Jenista Mhagama lakini nimpongeze na Naibu wake wametupa ushirikiano sana, pale tulipowataka kwenye Kamati yetu wamekuja wametupa maelezo, niombe sana mliangalie hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini liko tatizo lingine la MSD. Tumefika sisi mpaka MSD wanadai pesa na inawezekana kabisa itafika wakati watashindwa kabisa hata kupakua mizigo bandaraini. Kuna pesa ambayo wanaidai Serikalini na kwa bahati nzuri Naibu Waziri wa Afya tulikuwa naye wakati tumeenda MSD na yeye aliahidi kwamba kile kiasi cha pesa kitatolewa. Niombe watekeleze ahadi yao ya kuwalipa MSD.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja. Nawatakia kila la kheri na kazi njema, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya Wizara ya Ardhi mwaka 2011/2012 Bunge lilipitisha matumizi ya kuanzisha mabaraza ya ardhi na nyumba Wilaya ya Matano na Tunduru ikiwa ni mojawapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Baraza la Ardhi la Nyumba halikuanzishwa na Serikali kutokana na bajeti ya Wizara kwa muda uliopangwa. Ndipo Halmashauri kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ikafuatilia Serikalini mipango hiyo ya uanzishwaji wa Baraza. Jibu lililotolewa ni kwamba Serikali kwa sasa haina uwezo wa kuanzisha Baraza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kwamba wananchi wa Tunduru wanapata taabu ya kusafiri kilometa 264 hadi Songea kufuata huduma za baraza. Halmashauri ikaona ni vema itoe jengo miongoni mwa majengo ya Idara ya Ujenzi na samani japo chache ili angalau Baraza liweze kufanya kazi. Je, ni lini Serikal itaajiri Mwenyekiti wa baraza la Ardhi la Wilaya ya Tunduru? Kwa
sasa Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Songea Mheshimiwa Norbet Ndimbo ndiye anaetembelea Baraza la Tunduru kila baada ya mwezi mmoja na mara nyingine miezi miwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali itaajiri watumishi na wahudumu wa Baraza? Kwa sababu sasa kuna mtumishi mmoja Bi. Vumilia Chipasura anafanya kazi ya Uhudumu, Ukarani na Uchapaji. Ikiwezekana basi, hata huyo kibarua aangaliwe kama ana sifa aajiriwe na aongezewe watumishi wengine kwani amejitolea kwa muda wa miaka miwili sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri Serikali ijenge jengo la kudumu kwa ajili ya Baraza la Ardhi badala ya kuazima jengo Halmashauri. Hii iendane na ununuzi wa thamani za Ofisi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu cha hotuba ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ukurasa wa 31 – 32 amezungumzia jukumu la kuanzisha na kusimamia Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya kwa lengo la kutatua migogoro ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bajeti ya Wizara ya mwaka 2011/2012 Bunge lilipitisha matumizi ya kuanzisha Mabaraza matano ya Ardhi na nyumba ya Wilaya na Tunduru ikiwa ni mojawapo. Hadi sasa Halmashauri imetoa jengo miongoni mwa majengo ya Idara ya Ujenzi na samani japo chache ili angalau Baraza lianze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Waziri anapohitimisha michango mbalimbali ya Wabunge naomba mambo yafuatayo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iajiri Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya ya Tunduru kwa sababu kwa sasa mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Songea Mheshimiwa Norbet Ndimbo ndiye anayetembelea Baraza la Tunduru kila baada ya mwezi mmoja na mara nyingine baada ya miezi miwili. Hili halileti tija kwa wananchi wa Tunduru.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iajiri watumishi na wahudumu wa baraza; kwa sasa kuna mtumishi mmoja tu Bi Vumilia Chipasura, anafanya kazi kama kibarua, hajaajiriwa na anafanya kazi zote za uhudumu, ukarani na uchapaji, ikiwezekana hata huyo aajiriwe.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ijenge jengo la kudumu kwa ajili ya Baraza la Ardhi badala ya kuazima jengo Halmashauri, hii iendane na ununuzi wa samani za ofisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kuwa si vizuri kuendelea kuanzisha mabaraza mengine ya ardhi na nyumba ya Wilaya ikiwa haya yaliyopitishwa na Bunge hayajakamilika.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia siku ya leo, na hasa katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani ambapo waislamu wote kote nchini wanatimiza miongoni mwa nguzo tano zile ni pamoja na kufunga Ramadhani. Namshukuru Mungu, nawatakia kila la heri wale wote ambao wamewajaliwa kutimiza nguzo hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa dhati ya moyo wangu na kama sikusema haya hakika sitaietendea haki nafsi yangu, naomba binafsi nikupongeze sana kwa kazi nzuri unayoifanya. Kuna usemi wanasema usimdharau usiyemjua. Awali wakati unaingia kwenye nafasi hii nilipata shida sana kuona kweli Naibu Spika utamudu nafasi hii! Kwa kweli, umeitendea haki nafsi zetu, lakini umetufurahisha akinamama wenzako, hakika unatuwakilisha vizuri endelea kuchapa kazi tuko pamoja na wewe na Inshallah tunakuombea uendelee kuwa salama mpaka tarehe Mosi tunapomaliza kufunga Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana niwapongeze, Waziri wa Fedha na Naibu Waziri, wamewasilisha mpango mzuri na wametupa nafasi hata sisi Wabunge ya kuona nini kimeandaliwa katika bajeti hii. Naomba niwapongeze sana kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini yako mambo mengi yamezungumzwa mazuri. Miongoni mwa mambo mazuri lazima kuwe na changamoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie upande wa afya. Waheshimiwa Wabunge, wenzangu wengi wamezungumzia kuhusu ujenzi wa vituo vya afya na zahanati, niwapongeze sana na mimi nakubaliana nao moja kwa moja, lakini mimi naomba sana nizungumzie suala la ikama ya watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakuwa shahidi na Mheshimiwa Waziri anayehusika atakuwa shahidi kwamba tunalo tatizo la watumishi wachache katika Idara hii ya afya. Mimi niombe sana tuliangalie jambo hilo, kwa kuwa tunalo tatizo la hawa watumishi ni vizuri kupitia vile vijiji vyetu wako kule vijana ambao wamejifunza uhudumu wa afya, ni vizuri tukawaangalia wale kuwapa mafunzo, ili wawe wanasaidia kutoa huduma za afya kwenye zahanati na vituo vya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiofichika, hata tukienda sasa hivi kwenye vijiji vyetu unaweza ukakuta mhudumu mmoja, huyo huyo ataandika cheti, huyo huyo atachoma sindano, huyo huyo ataenda kuhudumia kusafisha vidonda, kazi zote anatakiwa azifanye. Kwa hiyo, mimi binafsi niliona sana kulingana na muda huu mfupi nijikite sana kwenye eneo hili katika kuhimiza kupata watumishi wa afya kwenye vituo vya afya na zahanati zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo naomba nilizungumzie ni suala la miradi ya maji. Tumekuwa tukizungumza sana kuhusiana na suala la miradi ya maji, siyo siri iko miradi ambayo tayari wananchi wetu wamekabidhiwa, lakini upo ukweli usiofichika kwamba, miradi ile mpaka sasa iko miradi mingine haifanyi vizuri, haitoi maji ipasavyo. Mimi naomba sana, kupitia Wizara husika, ufanyike uhakiki wa kuona ni miradi gani ambayo imekabidhiwa kwa wananchi, lakini haitoi maji ipasavyo kuona sasa hatua zichukuliwe katika kuhakikisha tunaifanyia ukarabati na wananchi wetu wanapata maji ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yamezungumzwa mambo mengi, lakini naomba pia nizungumzie suala la kupunguza tozo kwa wakulima. Kwenye taarifa yao wamezungumza na hasa kwenye suala la wakulima wa korosho. Kama alivyoeleza Mheshimiwa Dkt. Mpango katika mpango wake kwamba watahakikisha wanapunguza tozo mbalimbali kwa wakulima na mimi nakubaliana nao kwa sababu, zipo tozo ambazo zilikuwa zinawakandamiza sana wananchi wetu. kwa kuwa wameanza kupunguza baadhi ya tozo nasisitiza sana waendelee kuziangalia hizo tozo ambazo hazina maslahi kwa wananachi wetu, ni vizuri kuziondoa ili wakulima waone waone tija ya kile wanachokifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la bajeti. Hapa tunazungumzia bajeti tumeweka mipango mingi ambayo tunakusudia tupige hatua, lakini kama hatujasimamia ukusanyaji mzuri wa mapato, mimi naamini haya yote tunayozungumza hayawezi kuzaa matunda. Mimi nasisitiza sana kwenye haya mambo ambayo tumekusudia kwenye hivi vyanzo vya mapato ni vizuri tuvisimamie ili hii miradi ambayo tunaikusudia ifanyike, ifanyike kwa jitihada na itafanyika vizuri kama kile ambacho tumekusudia kukikusanya kitakusanywa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la bajeti. Hapa tunazungumzia bajeti tumeweka mipango mingi ambayo tunakusudia tupige hatua, kama hatujasimamia ukusanyaji mzuri wa mapato naamini haya yote tunayozungumza hayawezi kuzaa matunda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninasisitiza sana katika haya mambo ambayo tumekusudia katika vyanzo vya mapato ni vizuri tuvisimamie ili hii miradi ambayo tunaikusudia ifanyike, ifanyike kwa jitihada na itafanyika vizuri kama kile ambacho tumekusudia kukikusanya kitakusanywa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie jambo…..

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na ninaunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya mimi kuungana na Wabunge wenzangu katika kuchangia bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasahau, naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri anayoifanya. Sote tunafahamu kwamba Rais wetu Magufuli ni binadamu kama binadamu wengine. Kila binadamu anapofanya jambo jema anapenda kupongezwa na kwa kufanya hivyo tunampa nguvu katika kutekeleza majukumu yake. Naomba niungane na Wabunge wenzangu lakini niungane na wananchi wote kwa ujumla, kwa kweli tunampongeza sana Mheshimiwa Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya na niseme binafsi naendelea kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ili afanye kazi yenye kuleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Halmashauri. Kwa bahati nzuri mimi ni Mjumbe wa ALAT- Taifa. Kama tunavyofahamu kwamba Mkutano wa ALAT-Taifa unaunganisha Wenyeviti wa Halmashauri, Mameya, Wakurugenzi lakini wamo na Wabunge kutoka katika kila Mkoa. Mimi ni Mbunge ambaye nawakilisha ALAT-Taifa kutoka kwenye Mkoa wangu wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa sababu kupitia kikao ambacho kilifanyika tarehe 22 - 24 Septemba, 2016 mkutano ambao ulifanyika Mkoa wa Mara, kupitia Halmashauri zetu mambo mengi sana waliyazungumza. Miongoni mwa mambo ambayo yalizungumzwa ni pamoja na Halmashauri nyingi kukosa watendaji walioajiriwa wa kada mbalimbali. Jambo hili limezungumzwa sana na Wabunge wenzangu na mimi nimeona ni bora nisisitize kwamba wakati sasa umefika kuhakikisha tunaajiri watendaji katika kada mbalimbali ikiwemo Watendaji wa Vijiji, Watendaji wa Kata na wale wakuu wa idara ambao wanafanya kazi moja kwa moja katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lilizungumzwa ni kuchelewa kupelekwa kwa peza zile za vyanzo vilivyofutwa. Tatizo hili limekuwa sugu, nimeona ni bora nisisitize jambo hili kwamba wakati sasa umefika wa kuhakikisha vyanzo vile ambavyo tulivifuta tunapeleka pesa kwa wakati. Kwa kufanya hivyo, tutazisaidia Halmashauri zetu kutekeleza majukumu ambayo yamepitishwa kupitia bajeti za ngazi ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuchelewa kupelekwa kwa OC. Hili jambo naomba nilizungumze na naomba nitolee mfano kwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, toka mwaka jana mwezi Julai OC katika idara zile mbalimbali hazijaenda. Naomba kuisisitiza Serikali tupeleke OC katika zile idara kwa kufanya hivyo tutazisaidia idara zetu kutekeleza majukumu yake kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba niliseme tena kabla sijasahau na kwa umuhimu wake, naomba nizungumzie barabara kwa kiwango cha lami inayotoka Mbinga-Mbamba Bay. Napozungumzia Mbamba Bay maana yake naigusa Wilaya ya Nyasa. Sote tunafahamu kwamba Wilaya ya Nyasa ni miongoni mwa Wilaya zilizoko mpakani. Wilaya hii inapaswa sasa kuona umuhimu wa kutengenezewa barabara kwa kiwango cha lami. Tunafahamu matatizo ambayo yanaweza yakajitokeza kwenye barabara za mipakani.

Kwa hiyo, ni vizuri kuhakikisha tunatengeneza barabara hiyo kutoka Mbinga mpaka Nyasa kwa kiwango cha lami. Nimeona niliseme hili nikiwa nafahamu kwamba mara nyingi hata watumishi wanaopelekwa kwenye barabara hizi za mpakani wamekuwa na wasiwasi na hasa wakiangalia masuala ya miundombinu. Naomba nisisitize Serikali yangu katika kuhakikisha tunakamilisha ujenzi wa barabara ya lami kwa kiwango cha lami kutoka Mbinga mpaka Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naomba nilizungumzie ni suala la shilingi milioni 50. Wenzangu wengi wamelisema na wengine wamekuwa wakifananisha na mamilioni ya Mheshimiwa Jakaya Kikwete. Mimi naomba niseme hizi shilingi milioni 50 zilikuwa ahadi kutoka kwa Rais wetu aliahidi baada ya ushindi wa chama chetu na sina shaka kwamba tulishinda kwa kishindo na mimi nachofahamu utamaduni wa Serikali yetu ya Awamu ya Tano ni kutekeleza kile tulichoahidi, niombe sana tutekeleze kwa kupeleka hizi shilingi milioni 50. Nafahamu tunapozungumza Serikali za Vijiji ni mamlaka kamili zina Wenyeviti, Halmashauri za Vijiji na zina Wenyeviti wa Vijiji, tupeleke hizi pesa wao sasa wataona ni nini kifanyike kupitia hizi shilingi milioni 50. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo mimi naomba nilizungumze hapa, ni suala la vifo vya akina mama wajawazito, naguswa sana na jambo hili nikiwa mimi ni sehemu ya wazazi. Tumelisema sana akina mama kupitia kwenye vikao hivi lakini kinachosikitisha zaidi hata ukiangalia kwenye bajeti zetu jambo hili linaonekana halipewi kipaumbele. Mimi nimeona niliseme hili kwa huzuni kubwa sana nikiwa nafahamu kwamba ninapozungumzia suala la vifo vya akina mama wajawazito ziko sababu nyingi zinazosababisha vifo. Sababu mojawapo ambayo mimi nimeiona ni ukosefu wa vifaa tiba. Mpaka hivi tunavyozungumza kwenye zahanati zetu akina mama wanatakiwa waende na mabeseni na vifaa vya kujifungulia. Sisi kama Serikali wakati sasa umefika mama anapokwenda kwenye kituo vile vitu anavikuta hapo hapo kwenye zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ni suala la wataalam. Tumezungumza sana suala la kuajiri watumishi wenye ujuzi wa kutosha katika zahanati zetu. Ni jukumu langu kama mama kusisitiza kwamba sasa wakati umefika wa kuona tunakuwa na wataalam wa kutosha kwenye maeneo ambayo wakina mama wanajifungulia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni maeneo ya kutolea huduma. Napozungumzia maeneo ya kutolea huduma nagusa zahanati na vituo vya afya. Waheshimiwa Wabunge wenzangu mtakuwa mashahidi tuliahidi kujenga zahanati kila kijiji na kujenga kituo cha afya kila kata. Naomba sana wakati sasa umefika wa kutekeleza na ni vizuri sasa kwa kuwa Serikali hii sikivu basi ni bora na wananchi wetu waone inasikia kwa vitendo, itekeleze vile vitu ambavyo imeahidi na mimi naamini kwa kufanya hivyo itaturahisishia hata katika kipindi kijacho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo mimi naomba niliseme na kweli wenzangu wengi wamelisema ni suala la miradi ya maji. Tunayo miradi ya maji ambapo mpaka hivi tunavyozungumza haileti tija kwa wananchi wetu. Kama tunavyofahamu wahanga wakubwa wa jambo hili ni akina mama. Tumtue mama ndoo, tukaribishe huduma hii kwa mama, hivi tunavyoona akina baba wanapendeza, wamevaa suti nzuri ni kazi ya sisi akina mama katika kuhangaika kutafuta maji. Kwa hiyo, mimi kama mama, kama mwanamke ambaye na mimi ni miongoni mwa waathirika wa jambo hilo ninalazimika kusisitiza Serikali kwamba wakati umefika wa kuhakikisha tunatenga bajeti za maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi iko mingi lakini miradi mingine ni viporo na kwa kuweka miradi viporo tunaisababishia ile miradi kuongezeka gharama za uendeshaji. Kwa hiyo, kupitia kikao hiki nisisitize sana, iko miradi mingine mpaka hivi tunavyozungumza ilikabidhiwa kwa wananchi, lakini haitoi maji, wakati sasa umefika kwa Serikali yetu kuona uwezekano kupitia Halmashauri zetu kubaini miradi yote ambayo haijatekelezwa ipasavyo lakini kuitengea pesa miradi mipya ya maji kuhakikisha tunaondokana na hili tatizo la miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake. Katika kipindi ambacho nimekaa hapa Bungeni, miongoni mwa Wizara ambazo zimetulia ni pamoja na Wizara hii. Dalili ya kuonyesha Wizara hii imetulia ni kusikilizana kwa Waziri na Naibu wake lakini kama hiyo haitoshi kusikilizana kwa Waziri, Naibu na watendaji katika Wizara. Mimi naamini kwenye Wizara mkiwa na wimbo mmoja kila kitu kitafanikiwa. Mnafanya vizuri, binafsi nawapongeza sana na naendelea kuwatia nguvu, endeleeni kufanya kazi, endeleeni kuchapa kazi sisi tunawatumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana kwa suala la kuondoa ushuru wa mazao ya chakula. Miongoni mwa vitu ambavyo vilikuwa vinawagombanisha viongozi na wakulima ni suala la ushuru ilikuwa shida sana katika Halmashauri yetu. Mimi naona katika vitu ambayo mmeitendea haki Serikali yetu, mmewatendea haki wakulima wetu ni katika kuondoa suala la ushuru kwamba sasa wakulima wameruhusiwa kusafirisha tani moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye hili eneo naomba tusije tukasahau, kwamba kupitia hapo hapo Halmashauri zilikuwa zinapata pesa. Nalisema hili kwa sababu nina uzoefu nalo, mimi kama mkulima naweza nikawa na tani zangu kumi, nitakachokifanya ili nisafirishe kwa kutimiza huu wajibu wa tani moja ni kuandika jina la mwanangu, mjomba wangu, shangazi ili kuhakikisha tani kumi zote zinasafirishwa. Kwa kuwa Serikali imeamua kuwarahisishia kusafirisha tani moja ni vizuri tuweke mkakati mzuri na tuziagize Halmashauri zetu ni mbinu gani zitatumika …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia leo kusimama katika Bunge lako hili kupata fursa ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kumshukuru Mwenyezi Mungu naomba pia niwashukuru akinamama wenzangu walioniwezesha kuingia katika Bunge hili, naahidi kuendelea kushirikiana nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, dada yangu Ummy, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara. Nawapongeza hawa nafahamu sana umuhimu wa Wizara ya Afya kwa Watanzania. Kazi inayofanyika na dada yangu Ummy na Naibu Waziri ni kazi nzuri sana inapashwa kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwa kuzungumzia masuala muhimu ambayo nakusudia kuyasema kwa siku hii ya leo. Niendelee kutoa pongezi. Katika Mwaka wa Fedha 2017/2018 mnamo tarehe 6 Agosti, nilitembelea Wilaya yangu ya Nyasa Mkoa wa Ruvuma. Nilishuhudia tukiwa tunapokea vifaa mbalimbali ikiwemo vitanda na vifaa vya upasuaji. Naomba sana nipongeze jitihada za Serikali hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. Imepelekea kufikia sasa kupata akina mama waliofanyiwa upasuaji kufikia 87.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni jitihada nzuri ya kuonesha kwamba tunaokoa maisha ya akinamama na watoto. Hata hivyo, liko tatizo kubwa katika hospitali ile, tatizo la X-ray. Nimwombe dada yangu Ummy amefanya mambo mazuri sana, naamini x-ray ni jambo dogo tu atalikamilisha, atujalie tupate x-ray katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la vifo vya akinamama wajawazito. Tunapozungumzia vifo vya akinamama wajawazito ziko changamoto nyingi ambazo zinapelekea kupatikana kwa vifo vya akinamama wajawazito. Mojawapo ya mambo ambayo yanayojitokeza ni umbali wa eneo la kujifungulia, vifaa tiba na wauguzi. Nafikiri hivyo ni miongoni mwa vitu ambavyo vinatakiwa viwepo kwenye hospitali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia suala la umbali wa eneo la kujifungulia kama nitakuwa na kumbukumbu nzuri kupitia ahadi za Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi tuliahidi kuwa na zahanati kila kijiji na kuwa na kituo cha afya kila kata. Niombe dada Ummy atakapofika basi atueleze, mimi kama mwakilishi wa akinamama wa Mkoa wa Ruvuma napenda kujua tumefikia hatua gani katika kuhakikisha ahadi hizi zinatekelezwa ipasavyo; na kupitia hivyo vijiji pia nitapata fursa ya kuona ni vijiji gani sasa kwenye Mkoa wangu wa Ruvuma tumefanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la wauguzi. Wachangiaji wengi wamesema kwamba tunalo tatizo la Ikama ya watumishi. Ziko zahanati ambazo mpaka leo ukienda unaweza ukakuta mhudumu mmoja tu. Nesi afanye kazi ya kuandika huyo huyo, nesi aende akampime mama mjamzito, nesi aende akazalishe mama mjamzito, nesi aende akatoe dawa. Kwa hiyo jambo hili ni muhimu sana niombe tuangalie sana katika suala hili la Ikama ya watumishi. Kwa bahati nzuri kupitia vitabu hivi wameeleza, kitabu cha Waziri amesema, kupitia zoezi lile la vyeti feki na mambo mengine ambayo yamejitokeza watumishi wengi sasa hawapo kwenye zahanati zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kuna usemi unasema ukikata mti panda mti, kwa hiyo tumaini langu kwamba tumewatoa wale watumishi ambao tunafikiri kwamba wa likuwa na makosa kwa namna moja au nyingine, ni wajibu wetu sasa kuona nafasi zile tunazifidia katika kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la upatikanaji wa dawa. Wamezungumza kupitia kwenye vitabu lakini nishukuru maoni ya Kamati ya Huduma za Maendeleo ya Jamii kupitia ukurasa wa 35, wamesema na wametoa mapendekezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye vitabu hivi unaona kabisa kwamba sasa suala la dawa si tatizo katika nchi yetu, lakini ukienda katika hali halisi yako maeneo mpaka hivi tunavyozungumza yana upungufu mkubwa sana. Wajumbe wa Kamati kupitia maoni ya Kamati wamesema ni vizuri sasa kama Wizara waweke utaratibu wa kuhakiki kuona hizi dawa zinaishia wapi kama kweli zinafika kwa watumiaji. Ni tatizo kubwa sana la upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu bahati nzuri alifanya ziara Mkoani kwetu Ruvuma, lakini miongoni mwa mambo ambayo alikumbana nayo ni upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja kufanya mkutano katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ilisikitisha sana pale alipomwomba Daktari aeleze dawa zilizopo. Vile alivyojaribu kumweleza wananchi walimzomea sana. Hii ni kuonesha kwamba hizi dawa tunazozungumza kwenye makabrasha pengine sio zile zinazofika moja kwa moja kwa wananchi. Niombe sasa Serikali yangu, naamini hii ni Serikali sikivu sana ione hivyo.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna njia nyingine yoyote, sisi uwepo wetu hapa umetegemea na afya zete; kama tusingekuwa na afya njema tusingekuwepo humu ndani leo. Sasa kuwepo na dawa itarahisisha sana kuona matibabu yanapatikana haraka sana. 0525

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala lingine la matibabu ya wazee. Naomba niseme; kwamba suala hili la matibabu ya wazee tumelisemea sana lakini mimi naweza nikaona halijasimamiwa ipasavyo. Hawa wazee tunaowazungumzia wanapokwenda kwenye hospitali si tu kuandikiwa dawa ni pamoja na kupata dawa. Kwa hiyo niombe huu mfumo ambao tunakusudia kutoa matibabu kwa wazee uzingatiwe vizuri ili wazee wale wafaidike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa sababu naamini na sisi wote ni wazee watarajiwa. Kwa hiyo tukiweka misingi mizuri leo hata sisi Mwenyezi Mungu akitujalia tukafika huko uzeeni tutanufaika na hii mipango ambayo tumekuwa tukiiweka. Nimwombe sana dada Ummy kwa kazi nzuri anazozifanya anawapigania akinamama lakini anazungumza sana suala la wazee, basi tuhakikishe wazee hawa wanapata huduma ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la vituo vya afya. Sisi katika Halmashauri yetu ya Tunduru; naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Tunduru kupitia wadau mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge; tumejitahidi pale katika kuhakikisha ujenzi wa kituo cha afya unaendelea. Hata hivyo, tuiombe sasa Serikali kuweka msukumo. Kama mnavyofahamu nguvu za wananchi peke yake zinaweza zisitoshe, kwa hiyo tunaiomba Serikali iangalie katika kuona tunaboresha kile kituo cha afya ili tuendelee kupata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kituo hicho cha afya ambacho nimekizungumzia kilichopo Kata ya Nakayaya pia naomba kituo cha afya kilichopo Kata ya Narasi. Pale tuliahidiwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, naamini Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hayupo lakini Serikali ya CCM ndiyo iliyopo madarakani. Tuliahidiwa pale kupata kituo cha afya; na kwa kweli ukiangalia na idadi ya watu waliopo pale tunastahili. Niombe sana katika kutekeleza jambo hili wakati utakapofika tunapoona umuhimu wa kuongeza vituo vya afya basi na kile kituo kipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la CHF; limezunguzwa kwenye vitabu na sisi sote tunalifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukihimiza sana wananchi wetu kujiunga na CHF, na bahati nzuri dada Ummy amelizungumza kupitia kitabu chake; kwamba wanakusudia kuwa na CHF ya pamoja ambapo mgonjwa itamwazesha kutibiwa kutoka kwenye kituo cha afya, atatibiwa hospitali ya wilaya na vile vile atakwenda kutibiwa mkoani. Naomba katika kutekeleza hili tuangalie na changamoto zilizojitokeza. Inawezekana tukawa tunaangalia tulipoanguka lakini tukasahau tumejikwaa wapi, hatimaye tumeanguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa sababu watu wengi wamekuwa wakisita kujiunga na CHF kutokana na huduma zinazotolewa. Mtu anajiunga kwenye CHF anapopata tatizo akienda kwenye zahanati hakuna dawa, hilo limekuwa tatizo. Sasa kwa kuwa tunakusudia kuwa na CHF ya pamoja, basi ni vizuri tukaangalia changamoto ambazo zimejitokeza katika mfumo huu tulipoanza nao ili tuboreshe ili wananchi wetu waweze kupata huduma zinazostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo jema na wengi kwa kweli walikuwa wakikata tamaa. Kwa mfano sisi katika Halmashauri yetu ya Tunduru ni wakulima wa korosho. Mtu anaweza akatoka Nalasi anakuja Makao Makuu ya Wilaya kuja kupokea pesa yake, lakini akiwa pale anapata tatizo la ugonjwa, CHF inafanya kazi katika zahanati yake, makao makuu ya wilaya haifanyi kazi. Kwa hiyo tukiweka mfumo mzuri itawasaidia, kwamba wanapopata matatizo hata kwenye hospitali za wilaya wanapata kutibiwa lakini watakwenda pia kutibiwa hospitali ya mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kusisitiza suala la upatikanaji wa dawa kama nilivyosema, ni kitu muhimu sana, naomba Mheshimiwa Waziri dada Ummy akizingatie sana. Inawezekana pengine taarifa hizi wanazozipata kupitia ngazi za mkoa zisiwe sahihi. Tukija kule kwenye maeneo yanayohusika pengine ile hali sivyo ilivyo, kwa hiyo nasisitiza jambo hili...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia tena kusimama tena katika Bunge lako hili Tukufu, naamini hili ni Bunge la pili kutoka mwisho, lakini namwomba Mwenyezi Mungu anijalie ili nirudi tena katika Bunge lijalo. Pia nawaombea na Waheshimiwa Wabunge wenzangu warudi tena maana si vizuri kujiombea mwenyewe peke yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipongeze taarifa ambazo zimewasilishwa siku ya leo, lakini naomba pia nipongeze michango mizuri ambayo imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu na hasa Wajumbe wa Kamati ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa karibu na hizi Wizara ambazo zimewasilisha leo taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo mambo machache ambayo naomba pia niseme, niweke nyongeza katika maeneo ambayo wenzangu wameyazungumza. Naomba nizungumzie suala la utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika halmashauri zetu. Nafahamu kwamba Serikali inapeleka pesa katika halmashauri zetu kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali kupitia force account, hiyo ni hatua nzuri na kwa kweli naomba niipongeze Serikali kwamba ilikuwa na lengo zuri sana kupitia force account.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisisitize suala la uhakiki wa miradi, tunaenda tunatekeleza hii miradi, lakini wakati mwingine pengine miradi inatekeleza kwa haraka sana inakuwa inakosa ubora. Unaweza ukakuta jengo limekabidhiwa kwamba limekamilika, lakini baada ya mwezi mmoja ukienda kuhakiki unakuta tayari lina ufa. Sasa kwa namna nyingine inaonekana kama pesa yetu imekwenda lakini haijafanya kazi kadri inavyokusudiwa. Kwa hiyo naomba sana nisisitize uhakiki wa miradi ambayo inatekelezwa katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kusisitiza kwamba mfumo huu ni mfumo mzuri kupitia force account lakini tuwe imara katika kuhakikisha miradi hii inayojengwa, basi hiyo ni miradi yenye ubora. Kama jengo linajengwa basi liwe jengo bora, kama ni kituo cha afya, kama ni madaraja na miradi mingine yote ambayo inatekelezwa katika halmashauri zetu iwe na ubora unaohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba nizungumze suala la vyanzo vya mapato. Katika halmashauri zetu sasa ni kama vyanzo vinaenda kwa kusuasua, naomba niseme kwamba Serikali ilikuwa na dhamira nzuri sana ya kufuta vyanzo vya mapato ambavyo vilikuwa vinakusanywa na halmashauri na kuleta kwenye Serikali Kuu, lakini kwa lengo la kurudisha pesa kwenye halmashauri ili ziendelee kufanya kazi ilivyokusudiwa. Naomba niseme na jambo hili nimekuwa nikisema lakini hata Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamelisema, kwamba pesa haziendi kwa wakati. Kutopeleka pesa kwa wakati ni kuifanya ile miradi isikamilike na tunapochelewa kupeleka pesa miradi ile inaongezeka gharama za uendeshaji. Kwa hiyo, naomba sana kupitia Bunge lako hili, ni vizuri tupeleke pesa kwa wakati ili halmashauri ifanye kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna suala la miradi viporo, kwenye halmashauri zetu tuna majengo mengi, majengo mengine nguvu za wananchi wanakuwa wamefyatua tofali kwa lengo la kuanzisha miradi na wakati mwingine ni maagizo ya Serikali kwamba lazima mradi unapokwenda kuwepo na nguvu za wananchi. Hivyo wananchi wanafyatua tofali kwa maana ya nguvu zao, maeneo mengine wanakusanya mawe, wanapeleka mchanga, lakini kukiwa kuna jengo limejengwa jengo halikamiliki kwa ajili ya kukosa pesa ambapo ndio mchango wa Serikali kwenye lile jengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana kupitia Serikali tuhakiki miradi yetu viporo, vinginevyo unaweza ukakuta majengo mengi saa hizi badala ya kufanya kazi iliyokusudiwa wanakaa popo au mengine wanalala mbuzi na mengine yanafanyika mambo ambayo hayakukusudiwa. Kwa hiyo naomba sana niisisitize Serikali yangu na sina shaka kwa kweli na Serikali yangu naamini ni Serikali sikivu, isikie iufanye uhakiki, vile ambavyo tunahakiki watumishi hewa, turudi sasa tuhakiki hata miradi viporo ili tupeleke pesa ile miradi ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naomba nilizungumze, ni suala la posho za Madiwani, wenzangu wamesema na mimi nafahamu ukiachia kwamba ukiwa Mbunge pia ni Diwani, lakini mimi pia nimekuwa Diwani toka huko nyuma, sasa nafahamu mazingira ambayo wanaishi Madiwani wetu kwenye halmashauri. Hili jambo limesemwa sana na linaposemwa sana na Waheshimiwa Wabunge wengi inaonesha kwamba jambo hili ni la halmashauri zote, Madiwani wetu hali zao sio nzuri, posho zenyewe hawapati kwa wakati, lakini mwingine amesema, Diwani anaweza akaenda amefanya kikao anapomaliza kikao hakuna anachosaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati naanza kujiombea hapa ili nishinde tena niliwaombea na wenzangu, lakini hata wale Madiwani kule pia tunawaombea, sisi hapa tumejaza, tukishajaza per diem, ukijaza Jumatatu per diem mpaka siku ya pili ya tatu hujaona mnaanza kuulizana, hapa nilikuwa nateta na jirani yangu vipi kuhusu utaratibu na naamini jambo hili ni kwa wote tunaulizana. Sasa vile tuone nafsi, lile ambalo sisi tunaliona sio jambo jema hata wenzetu kule haliwapendezi. Kwa hiyo, tuhakikishe Madiwani wetu wanapata pesa zao kwa wakati, wanadai na inaonekana wengine mpaka tutamaliza Mabaraza hata haki yao hawataipata. Sasa jukumu la kuhakikisha wanapata haki zao ni sisi tuliomo humu ndani, tuhakikishe wale wanapata haki zao kama vile ambavyo sisi leo tunaanza kuuliza utaratibu utakuwaje na ndio maana nimesema hili ni Bunge la pili kutoka mwisho, kwa hiyo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sikudhani Chikambo kuna taarifa Mheshimiwa John Heche.

T A A R I F A

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa kwamba ni kweli kwamba Madiwani hawana pesa na hawalipwi, lakini kuna baadhi ya Ma-DC wanaona kwamba Madiwani wakilipwa ni fever na sio haki yao, mfano mzuri ni DC wa Gairo anaona kwamba Madiwani wakilipwa sio haki yao na wanafanya kazi. Kwa hiyo anachozungumza ni sahihi Madiwani wanahitaji kulipwa pesa zao.(Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sikudhani unapokea taarifa hiyo.

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kuchangia. Kama nilivyosisitiza upande wa Madiwani, lakini pia tunapozungumza halmashauri tunaanzia ngazi ya kijiji hata Wenyeviti wetu wa Vitongoji, Wenyeviti wa Vijiji tumekuwa tukiyazungumza sana. Hii miradi tunayoizungumza hapa inaenda kutekelezwa kwenye vijiji, lakini unamkuta Mwenyekiti wa Kijiji, Mwenyekiti wa Kitongoji hapati chochote, hawezi kufanya kazi kwa sababu hakuna motisha yoyote. Kwa hiyo, niombe sana tunapowafikiria Madiwani lakini pia hata viongozi wetu wa ngazi zile ambazo ndiko tunakoenda kufanya kazi ni lazima tuwafikirie.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niyaseme hayo, lakini kwenye suala hili la posho nimalizie kwenye matatizo ambayo yanajitokeza kwenye halmashauri. Tunafahamu kwamba miradi yote ambayo tunapeleka kwenye halmashauri wahakiki wa miradi ni Kamati ya Fedha, ndio inatakiwa ikahakiki miradi kwa niaba ya Baraza zima, lakini inasikitisha Kamati ya Fedha mnaweza mkakaa hata miezi mitatu haijaenda kwenda kuhakiki miradi, sasa nani atajua ubora, nani ataleta changamoto kwenye halmashauri, hiyo inaleta tabu. Wakati mwingine inaonekana halmashauri zingine wanapeleka Madiwani au Kamati ya Fedha kwenda kuhakiki ni kama funika kombe mwanaharamu apite, kuna utaratibu wa kutaka ile Kamati ikahakiki, lakini unaiambia Kamati ya Fedha iende ikahakiki siku moja, hivi kweli itapitia miradi yote ikamaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara itoe tamko kwa ngazi ya halmashauri, ni vizuri kama haya mambo yako kwa mujibu wa Katiba au kwa mujibu wa sharia, basi tuagize halmashauri wahakikishe wanatekeleza kwa mujibu wa utaratibu kwa sababu kupeleka pesa ni hatua nyingine, lakini pia hata kuhakiki ubora wa miradi yetu ni jambo lingine. Nimeona niliseme sana kwa sababu mimi ni sehemu ya Madiwani, naona madhara yanayojitokeza kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo hata wenzangu wamelizungumza ni suala la TARURA. Naomba niipongeze Serikali wazo lilikuwa zuri la kuweka TARURA, inawezekana kukawa na wazo zuri lakini katika utekelezaji tukabaini changamoto. Mimi binafsi changamoto mojawapo ambayo naiona ni watu wa TARURA kutokuwa sehemu ya halmashauri, wanaenda kwenye halmashauri pale wanapoalikwa, si kama vile ilivyokuwa nyuma, kwa sababu mimi kama Diwani kuna shida mradi unategemea ninavyokwenda kwenye Baraza la Madiwani ndipo ambapo nitaenda kusema kulingana na barabara yangu, kulingana na zahanati yangu lakini ukija kwenye masuala ya barabara wale watu wa TARURA sio sehemu ya halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba sana Serikali yangu narudia kusema ni Serikali tukufu na Serikali sikivu ni vizuri sasa ione uwezekano watu wa TARURA wawe sehemu ya Wakuu wa Idara katika halmashauri zetu ili wa-report taarifa zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nami napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kusimama katika Bunge hili na kuungana na Wabunge wenzangu katika kujadili bajeti ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijafanya hivyo, naomba kwanza niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na viongozi wote katika Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi, naomba niseme kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajadili bajeti ya mwaka 2019/2020, tunajadili Makadirio ya Mapato na Matumizi katika kipindi hicho cha 2019/2020, lakini tukiwa tunafanya hivyo, tumepitisha bajeti mbalimbali huko nyuma. Nimesimama hapa kwa ajili ya kutaka kumkumbusha Mheshimiwa Waziri, tukiwa tunataka kupiga hatua katika mwaka wa fedha huu 2019/2020, ni vizuri tukaangalia bajeti hizo za nyuma, ni mambo gani tuliyajadili hapa lakini hayakupata ufanisi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mbalimbali ambayo tumeyajadili ikiwemo miradi ya maendeleo, lakini kwenye miradi ya maendeleo yako maeneo hatukufanya vizuri. Sasa ni jukumu letu kama Serikali, kujipima na kuona sasa tunapotaka kupita hatua, ni lazima tuangalie yale mambo ambayo tumeyapitisha huko nyuma na hayakufanya vizuri. Kwa mfano, tulijadili masuala mbalimbali yanayohusu ujenzi wa madarasa, ujenzi wa zahanati na majengo mbalimbali ambapo wananchi wetu wamekuwa wakijitolea. Wamefanya hizo kazi lakini iko miradi mpaka hivi nilivyosimama hapa, bado hatujafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, ni vizuri tukajipima kwa kuangalia kile tulichokifanya. Kwa nini nasema hivyo? Nasema hivyo kwa sababu katika hiyo miradi yako maeneo mengine ambayo wananchi wetu wamekuwa wakidai fidia mbalimbali. Niseme tu, katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, yako maeneo ambayo wananchi wetu wamekuwa wakipisha miradi hiyo ifanyike na miradi hiyo imekuwa ikigusa makazi yao. Kwa mfano, tulikuwa tunatekeleza mradi wa barabara kwa kiwango cha lami, barabara ambayo ilikuwa inaanzia Namtumbo – Kilimasela – Tunduru - Nakapanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza miradi hii wako wananchi ambao walitakiwa wapate fidia zao lakini mpaka hivi ninavyosema hawakupata fidia na ninaomba nieleze, wananchi wale wako katika makundi yasiyopungua manne, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize. Liko kundi la kwanza ambapo wananchi walilipwa fedha katika kutekeleza mradi ule wa barabara kwa kiwango cha lami, lakini walihisi kwamba wamepunjwa, Serikali ilitoa tamko kwamba hawasitahili kulipwa walichopata ni kile kile ambacho ni halali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo kundi la pili, wananchi walivunja nyumba kabla ya kupewa notice, Serikali ilisema kwa kuwa walivunja kwa hiari yao haiwezi kuwalipa. Liko kundi la tatu ambapo wananchi walipewa notice, kabla ya kufanyiwa tathmini walivunja nyumba zao. Serikali ilitoa tamko kwamba wangeweza kupata kifuta jasho au kifuta machozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo kundi lingine la nne ambalo mimi binafsi nimesimama hapa na linanisikitisha zaidi na ninaomba Serikali ilifanyie kazi. Kundi hili, wananchi walifanyiwa tathmini, walipofanyiwa tathmini, walionekana kwamba wanastahili kulipwa na waliingia kwenye mpango wa kulipwa, lakini wakati wa malipo walirukwa. Sasa nimesimama katika kuwasemea hawa wananchi. Nafahamu tuko hapa, pamoja na kazi zote za Mbunge, lakini ni pamoja na kuwasemea wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupitia Serikali, kama wapo ambao wanastahili kulipwa basi walipwe. Kwa sababu kila siku wanapokuja kufuatilia, wakati mwingine wanaambiwa anayestahili kulipwa mmoja. Wakati mwingine wanaambiwa wanastahili kulipwa wawili, wakati mwingine wanaambiwa wote hamstahili kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, kwa sababu wale walikubali kufanya hivyo, nami nafahamu wakati tunatekeleza miradi ya maendeleo, iko miradi ambayo inategemea fedha za ndani, lakini iko miradi ambayo inategemea fedha za wafadhili. Katika fedha za wafadhili kunakuwa na masharti ambayo wanayaweka katika mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia barabara hii wakati inajengwa, maelekezo ilikuwa kwamba suala la fidia ni suala la Serikali yenyewe, kwa maana ya mapato yetu ya ndani. Sasa kinachosikitisha zaidi, barabara hiyo tayari imeshafunguliwa. Mheshimiwa Rais bahati nzuri alitembelea kule kwetu karibuni, katika Mkoa wetu wa Ruvuma, alipokuja kule wananchi walijiandaa pale kutaka kushika mabango, lakini viongozi wakawaambia msishike mabango, wakakubali wakaacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba, kwa kuwa tunakusudia kupiga hatua, ni vuzuri tukaangalia viporo tulivyoviacha nyuma. Wananchi wangu wamekuwa wakilalamika, na siyo barabara hiyo tu, yako maeneo mengine wananchi wanapisha mashamba yao, wanaacha mashamba yao wanapisha Serikali miradi iendelee, lakini mwisho wa siku wanahangaika kila siku maofisini, wanadai fidia zao na hawapati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, nami nimepata habari kwamba miongoni mwa vitu ambavyo Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango havipendi ni kutokulipwa wananchi wetu. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, kama kweli tathmini imefanyika na wako ambao wanastahili kulipwa, basi ni vizuri jukumu la Serikali kuwalipa wale wananchi ili tuwatie moyo. Mwisho wa jambo hili ni mwanzo wa jambo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuongea hayo, kwa kweli nilisema kama sitaongea hayo inawezekana ningepoteza fahamu, kwa sababu nilikuwa na hamu kweli ya kuongea jambo hili kwenye Bunge ili lifanye utekelezaji na wananchi wale naamini watakuwa wananisikia, kwa sababu ndicho walichotuagiza tuje kuwasemea. Kuwasemea siyo tu kuhimiza miradi ya maendeleo, lakini kuwasemea pia na kuangalia kero zile ambazo wanazipata wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba nizungumzie suala la Halmashauri. Mimi kabla sijawa Mbunge, nimekuwa Diwani katika vipindi vinne kwenye Halmashauri. Naelewa vizuri sana masuala ya Halmashauri. Halmashauri zilizopo leo kwenye maeneo yetu ni tofauti na huko nyuma. Hali za Halmashauri zetu siyo nzuri. Tulifuta baadhi ya vyanzo vya mapato, tukawa tumeahidi kwamba Serikali itakuwa inafidia vile vyanzo. Kwa sasa ni kama haviendi kabisa. Kwa maeneo ambayo tunapeleka hivyo vyanzo, basi haviendi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba vile vyanzo ndivyo ambavyo Halmashauri wanakaa wanapanga bajeti kupitia vile vyanzo. Wanaangalia miradi ya maendeleo. Kutopeleka fedha kwa wakati maana yake ni kuzifanya zile Halmashauri zizidi kudidimia na kutoendelea na ile miradi ambayo wameipanga kwenye Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, sisi ni Wabunge, lakini tukiwa kwenye Halmashauri sisi pia ni Madiwani. Tunaona matatizo ambayo wanayapaya Madiwani wetu kwenye Halmashauri. Ziko Halmashauri, Diwani inafikia mpaka miezi kumi hajapata posho yake wala hajapata stahili yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linakatisha tamaa. Sisi tunakaa huku miezi mingi, lakini shughuli nyingi za kwenye Halmashauri wanafanya Madiwani wetu. Ni vizuri sasa Serikali ione uwezekano wa kupeleka fedha kwa wakati ikiwepo kuwatia moyo hao Madiwani nao wawe wanapata posho kama tunavyppata sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme, sisi tunao utaratibu, ikifika siku ya Jumanne, mtu anaangalia kama kuna chochote kimeingia, Jumatano, Mbunge anaangalia kama kuna chochote kimeingia, lakini kama hakikuingia tunaanza hapa; hatujapata, hatujapata, posho, haijatoka, haijatoka. Sasa kama jambo lile linakuuma wewe, lazima urudi umwangalie na mwenzio nyuma kwamba naye linamuuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tumetangulia, tumesimama mbele lakini huko nyuma wako wenzetu wanaotufuata. Wanaotufuata ni pamoja na Madiwani. Kwa hiyo, nilikuwa niiombe Serikali, tuangalie Madiwani, hali zao siyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la Madiwani, waliingia hata kwenye bima za afya. Naomba nikwambie, ziko Halmashauri mpaka sasa zinashindwa kulipa hata bima za afya za wale Madiwani. Wanakwenda kutibiwa wanaambiwa bima yako haisomi. Sasa vitu kama hivi vinakatisha tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeyasema haya kwanza nikiwa naamini kwamba mimi ni sehemu ya Madiwani. Pia kuna suala la mikopo, wamekopa ile mikopo, kwenye mabenki hawalipi. Sasa mwisho wa siku kile ambacho walistahili kukipata hawatakipata na wanafanya hivyo siyo kwamba Wakurugenzi hawapendi kufanya, uwezo unashindikana, kwa sababu tulichukua vile vyanzo, lakini katika kuchukua vile vyanzo tuliahidi kwamba tutarudisha, hatupeleki kwa wakati, hali imekuwa ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niyaseme haya na ninarudia tena mimi ni sehemu Madiwani, lakini yako mambo ambayo tunajadili kwenye Halmashauri kama hivyo nilivyosema miradi ya maendeleo, kama hatupeleki fedha kwa wakati ile miradi haiwezi kufanikiwa. Haiwezi kufanikiwa kabisa na Wabunge wenzangu wameyasema haya; zahanati, vituo vya afya, madarasa, na miradi mingine, wananchi wamefyatua tofali kwa nguvu zao, lakini leo tofali zimegeuka kuwa vichuguu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inatia huruma sana kama Serikali, kama Wawakilishi, wasingeweza kuja wote, sisi tumekuja kuwasemea. Naiomba Serikali yangu sikivu isikie maneno haya ninayoyasema hatimaye itekeleze.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja mia kwa mia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema na kupata fursa ya kuchangia bajeti hii ya Wizara. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia bajeti ya Wizara naomba kwa dhati ya moyo wangu niishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kufanikisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, barabara inayotoka Dar es Salaam mpaka Tunduru - Namtumbo
mpaka Songea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilihisi sitaitendea haki nafsi yangu kama zitazungumza jambo hili. Kwa dhati ya moyo wangu napenda sana niishukuru sana Serikali hii, kwa kipindi cha nyuma tumekuwa tukipata shida sana, wananchi walikuwa wakisafiri kwa muda mrefu, lakini kwa sasa inaleta faraja. Kwa kufanya hivyo, inachangia hata vyombo vya usafiri kuwepo na ushindani, tumekuwa na magari mazuri na wananchi wananeemeka na wanaahidi kuendelea kukiunga mkono Chama cha Mapinduzi katika siku zijazo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la Wabunge wa Viti wa Maalum kutokushiriki katika Kamati za Fedha. Toka nimeingia kwenye Bunge hili nimekuwa nikisikiliza Wabunge wenzangu wakieleza masikitiko yao. Kwa bahati nzuri, mimi nimekuwa Diwani katika vipindi vinne na
nimemaliza nikiwa Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri, naielewa vizuri sana Halmashauri. Nilikuwa Diwani wa Viti Maalum lakini nilikuwa Mjumbe katika kikao cha Kamati ya Fedha.
Mheshimiwa Spika, nimesema nilizungumze hili kwa sababu tumekuwa tukizungumza masuala mengi yanahusu akina mama, masuala ya mikopo, maji na mambo mengine.
Ili sisi Wabunge wa Viti Maalum tupate fursa nzuri ya kuchangia masuala haya, ni lazima tuwe Wajumbe wa Kamati ya Fedha, nasema Kamati ya Fedha kwa sababu nafahamu ndio kamati mama katika Halmashauri. Masuala yote tunayozungumza ni lazima yaanzie kule. Tunapokuja kwenye vikao vya Baraza la Madiwani ni kama Bunge, kunakuwa na dakika za kuchangia. Kwenye Kamati ya Fedha kama sijaelewa jambo lolote linalohusu mama mwenzangu ambapo mimi namuwakilisha, ninayo fursa ya kuomba kuchangia mpaka pale ninapoelewa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anayehusika kwenye hii Wizara, na mimi naanza kupata shida kwenye hii Wizara sijui kwa sababu Waziri ni mwanaume na Naibu Waziri ni mwanaume. Mimi naamini wangekuwa akina mama wenzetu, tungekuwa tunawauliza wenzetu nyie mna nini na sisi? Sasa naomba niliache leo kwa Wizara inayohusika ili itusaidie na katika kutenda haki. Na
mimi naamini hata tukiwa kwenye vikao vya Bunge, sisi Wabunge wote ni kitu kimoja. Tumekuwa tukishiriki Kamati mbalimbali, tatizo ni nini kwenye Halmashauri? Naomba kupitia jambo hili, Mheshimiwa Waziri anayehusika atupe majibu kwa sababu tumekuwa tukisema sana.
Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwa majibu ambayo yamekuwa yakitolewa, hata kama angekesha kuyaeleza nisingeelewa, kwa sababu tunavyozungumza, Madiwani wa Viti Maalum wanaingia kwenye Kamati ya Fedha, iweje Mbunge wa Viti Maalum unamzuia asiingie
kwenye Kamati ya Fedha?
Mheshimiwa Spika, nakushukuru, lakini tunazungumzia sasa. Sasa alikuwa mwanamke, mimi sikuwa Mbunge. Nazungumzia sasa
ambapo nimemkuta Mheshimiwa Simbachawene. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie ukurasa wa 11. Kwenye ukurasa wa 11 wamezungumzia suala la usuluhishi wa migogoro. Wewe na hata Waheshimiwa Wabunge wenzangu watakuwa mashahidi kwamba kumekuwa na tatizo la migogoro ya wananchi katika maeneo yetu kati ya kijiji na kijiji, kati ya Wilaya na Wilaya; kati ya Mkoa na Mkoa; na kati ya wafugaji na wakulima. Hili jambo tumelisema sana kupita vikao vya Bunge na tuliambiwa kwamba imeundwa kamati ambayo itakuwa inashughulikia. Kamati zile tunatumaini zitafika kwetu.
Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutueleza, atuambie katika kusuluhisha na katika kuunda hizi Kamati ambazo zitahusisha Wizara tano, atuambie wamefikia wapi, ili tupate majibu. Kama hawajafikia ni vizuri sasa hatua zichukuliwe kwa sababu hali
ya migogoro kati ya wakulima na wafugaji sio nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie tena suala la afya. Kwenye suala la afya kwenye ahadi yetu ya Chama cha Mapinduzi tuliahidi kujenga zahanati kila kijiji, lakini tuliahidi kujenga kituo cha afya kwenye kila Kata. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja atuambie mpaka sasa tumefikia wapi? Pamoja na kwamba hii ahadi ni kwa kipindi cha miaka mitano, lakini lazima tuoneshe hatua, tumefikia wapi? Nilikuwa naomba anapokuja atueleze sasa tumepata vijiji vingapi ambavyo vina zahanati na tumepata kata ngapi ambazo zina vituo vya afya.
Mheshimiwa Spika, katika kutenda haki, tumeunda Mabaraza ya Kata na kwenye Vijiji vyetu, lakini mabaraza yale ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakishughulikia migogoro ya wananchi, wale Makarani hawajaajiriwa na wameeleza.
Kwa hiyo, naomba tupate ufafanuzi, katika kutenda haki. Ili haya masuala ya rushwa tunayoyazungumza yasiwepo, ni lazima yule mtu awe ameajiriwa; kama hatujaajiri, tunawezaje kufanya kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo naweza kulizungumza ni suala la kukaimu watendaji kwenye vijiji vyetu na Kata. Tumesema sana kupitia kwenye vikao vyetu kwamba tunalo tatizo la kukaimu nafasi hizi, tunaomba sasa na wakati umefika wale kwenye vijiji vyetu tuwaajiri
watendaji; unapomwajiri mtu anakuwa na mamlaka kamili.
Kama hiyo haitoshi, hata Wakuu wa Idara, maeneo mengine Wakuu wa Idara hawajathibitishwa. Nilikuwa naomba kwamba kwa maana ya hao Wakuu wa Idara ambao wamekidhi vigezo, basi tuwathibitishe ili wafanye kazi wakiwa wanajijua kwamba wao ni Wakuu wa Idara kamili.
(Makofi)
Mheshimiwa Spika, nije katika suala la TASAF, Mheshimiwa Waziri, amekuwa akilizungumza vizuri sana na amegusa kwamba katika kipindi kilichopita amezungumzia kwamba umefanyika uhakiki wa kuangalia watu ambao walikuwa wanapata zile fedha ambao hawastahili.
Wameguswa watu wengine ambao wanastahili kupata pesa, ni vizuri Mheshimiwa Waziri anayehusika arudi aangalie upya, kwa sababu pesa zile zimelenga kusaida kaya masikini, ni vizuri arudi aangalie upya kuona kweli hizi takwimu tunazozipata ni takwimu sahihi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la mwisho ambalo naomba nilizungumze ni suala la kuongeza mamlaka za utawala.
Miongoni mwa Wilaya kongwe katika nchi hii ni pamoja na Wilaya ya Tunduru. Wilaya ile ilianzishwa mwaka 1905 na ina kilometa za mraba zisizopungua 18,000 yaani ukiichukua Wilaya tu ya Tunduru, ni sawa na Mkoa wa Mtwara. Imefika mahali wananchi wale wa Tunduru wanahisi kwamba siyo sehemu ya Tanzania kwa sababu eneo la utawala lile ni kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kwenye Wizara hiyo wakati unapofika, ni vizuri sasa wakaangalia kuona katika kugawa maeneo ya utawala na sisi kwenye Wilaya ile watufikirie katika ule Mkoa wetu wa Ruvuma. Wilaya ile ni kubwa. Katika kuhakikisha huduma za wananchi zinakuwa
karibu, ni vizuri sasa tuone uwezekano wa kugawa hizo Wilaya, lakini ikiwemo na Wilaya ya Tunduru. Kama Mheshimiwa Rais itampendeza na ninafurahi kwamba Wizara hii sasa iko chini ya Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa mchango wangu. Naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ya mimi kuungana na wachangiaji wenzangu katika kuchangia Wizara hii ya Kilimo na Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema. Sambamba na kumshukuru Mwenyezi Mungu, naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kujali muda naomba niende moja kwa moja ukurasa wa 22. Katika ukurasa huu Wizara imeendelea kuhimiza matumizi bora ya mfumo wa stakabadhi ghalani. Naomba nimpongeze sana Waziri na naweza nikasema kwamba Waziri Mheshimiwa Dkt. Tizeba amekuja na mguu mzuri kwenye Wizara hii kwa sababu miongoni mwa watu ambao wamenufaika na mfumo huu wa stakabadhi ghalani ni sisi wakulima wa korosho wa Mkoa wa Ruvuma na hususani wa Wilaya ya Tunduru na Namtumbo tumefaidika sana kupitia mfumo huu wa stakabadhi ghalani na ni imani yangu kwamba kupitia mfumo huu utawezesha sana kuwasaidia wakulima wa korosho katika maeneo yote ambayo tunalima korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haikuwa rahisi kuukubali mfumo huu kwa sababu kumbukumbu zangu zinaonesha mwaka 2011/2012 wakulima wa korosho Wilayani Tunduru na maeneo mengine tulitumia mfumo huu lakini mpaka hivi tunavyozungumza wakulima wale hawakupata pesa zao bado wanadai. Kwa hiyo, haikuwa rahisi kuukubali mfumo huu kutokana na hizo changamoto ambazo zimejitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti,Kwa nafasi ya pekee sana naomba sana nimpongeze Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma na watendaji wake kwa hakika walijitahidi sana kuelimisha wananchi hatimaye waliendelea kuelewa mfumo huu na hivi sasa tunavyozungumza naomba niseme kwamba umeleta tija sana kwa wananchi wetu na mimi ni miongoni mwa waumini wa mfumo huu nitaendelea kuhamasisha kama kiongozi kuhakikisha mfumo huu unaendelea kuleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tulikuwa na kikao cha wadau, kupitia kile kikao cha wadau kumetolewa tamko la kugawa sulphur bure. Ni jambo jema na ni jambo lenye tija lakini naomba Waziri alete mchanganuo na vigezo ambavyo vitatumika katika kutoa sulphur. Kwa kuwa jambo hili lina tija lisije likaleta migogoro baadaye. Hivi tunavyozungumza wako wakulima kwenye mashamba yao wanatumia kuanzia mifuko 10, 20 na zaidi sasa tulipotangaza sulphur bure inawezekana watu wakabweteka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Wizara inayohusika ikatoa mwongozo mapema kujua vigezo ambavyo vitatumika katika kutoa hiyo sulphur. Niliomba nisisitize hili na nilisisitize sana kwa sababu linagusa wananchi. Kama hiyo haitoshi naendelea kusisitiza kwa sababu wako wafanyabiashara ambao wamekuwa wakileta sulphur kutoka nje ya nchi kuwauzia wakulima wetu sasa wasije wakabweteka kwa kuamini kwamba Serikali sasa itatoa sulphur bure na wale wasilete sulphur matokeo yake tena badala ya kuimarisha zao la korosho tukaliletea tena matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha basi ni vizuri aeleze ili wananchi wale ajue kwamba mfumo na vigezo vitakavyotumika katika kutoa sulphur bure. Ni jambo jema, binafsi napongeza Serikali yangu na kwa kuwa Serikali hii ikitamka inatekeleza naamini itatekeleza lakini ni vizuri iweke mchanganuo watu wajue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la tozo. Binafsi naomba nipongeze sana. Tunapozungumzia hizi tozo moja kwa moja zilikuwa zinagusa wakulima wetu. Tunapopunguza hizi tozo maana yake tunapunguza mzigo kwa wakulima wetu, naipongeza Serikali na naomba niendelee kusema kwamba hata kama kuna tozo zile zingine ambazo zinaleta ukakasi kwa wananchi wetu basi waziondoe ili mazao yetu haya yaendelee kuwa na faida, kwa mazao yote kwenye korosho, kahawa na mazao mengine yote. Kama kuna tozo zile ambazo zinaleta kero kwa wananchi wetu basi ziondolewe ili kuleta faida ya kilimo bora kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la uvuvi. Kwenye eneo hili la uvuvi naomba nizungumzie Wilaya ya Nyasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia leo kupata fursa hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Maji, sote tunafahamu umuhimu wa Wizara hii kwamba maji ni uhai.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kumshukuru Mwenyezi Mungu, naomba nimshukuru sana Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazozifanya. Ukiangalia kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 126 na 127, wameeleza miradi mbalimbali ambayo itatekelezwa katika Mkoa wetu wa Ruvuma. Naomba niipongeze sana Serikali wametutengea shilingi 15,393,653,000, ni mkoa wa kwanza katika kutengewa pesa. Naomba sana niishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba niseme kutenga pesa ni hatua moja lakini kupeleka pesa katika miradi ni hatua nyingine. Niombe wakati utakapofika tupeleke hizi pesa ili kuhakikisha miradi ambayo tumekusudia kuitekeleza inatekelezwa. Miradi ambayo imepangwa kutekelezwa katika Mkoa wangu wa Ruvuma ni katika Wilaya za Madaba DC, Mbinga, Mbinga Mji, Namtumbo, Nyasa, Songea, Songea Manispaa na Tunduru. Kwa hiyo, naishukuru Serikali na niombe sana kwamba wakati utakapofika Mheshimiwa Waziri kama vile ambavyo umetuweka namba moja katika kututengea pesa nyingi basi ni vizuri katika utekelezaji vilevile tuwe namba moja katika kupeleka pesa.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spka, naomba pia nizungumzie Miradi ya Benki ya Dunia ambayo ilitakiwa itekelezwe katika Vijiji vya Mchoteka, Nakapanya, Majimaji na Muwesi. Naomba nimkumbushe Mheshimiwa Waziri anakumbuka hicho kitu kwamba miongoni mwa vijiji ambavyo viliwekwa kwenye mpango wa utekelezaji wa Miradi ya Maji ya Benki ya Dunia ni pamoja na hivyo vijiji ambavyo nimevisema. Niliwahi kusimama katika Bunge hili kuvizungumzia vijiji hivyo na Waziri alitoa majibu kwamba vijiji vile vimekosa vyanzo. Niombe, tafadhali Mheshimiwa Waziri naomba niseme kwamba vyanzo kule bado vipo. Ni vizuri sasa twende tukatekeleze katika kuona tunatafuta vile vyanzo vya maji kata hizi ambazo tunazifikiria kupata maji zipatiwe maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie tena suala la fidia Bonde la Mto Luhila - Songea. Mheshimiwa Waziri ninapozungumzia Bonde la Mto Luhila - Songea naamini utakuwa unakumbuka kwamba wananchi walipisha pale mradi mkubwa wa maji na hivi ninavyozungumza kiasi cha pesa karibu shilingi bilioni 1.9 wananchi wale wanadai. Imekuwa kero kwa sababu wananchi wale walikuwa wasikivu, walipisha huu mradi mkubwa, lakini mpaka hivi navyozungumza wananchi karibu 803 hawajapatiwa pesa zao. Nikuombe Mheshimiwa Waziri wakati utakapofika uhakikishe tunalipa fidia kwa wananchi wale ambao walijitolea kupisha mradi huu mkubwa wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie upatikanaji wa maji katika Miji Midogo ukiweno Miji ya Namtumbo na Lusewa. Naomba nizungumzie sana Lusewa hata ukija katika Kata ile ya Lusewa kuna kituo cha afya ambacho hakina maji. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, naamini bado mwanya upo, utufikirie katika kituo chetu cha Lusewa kutupatia maji. Tunapozungumza maji kama walivyosema Wabunge wenzangu sisi akina mama, watoto ndiyo hasa tunaathirika katika suala hili la maji. Tunapokuwa na kituo cha afya ambacho hakina huduma ya maji ni mtihani mkubwa sana. Nikuombe tufikirie sisi wananchi wa Mkoa wa Ruvuma na hususani wale wananchi waliopo katika Kata ile ya Lusewa wakati utakapofika ili tupate mradi wa maji katika Kijiji kile cha Lusewa. (Makofi)

Mheshimia Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia kusimama katika Bunge hili kuweza kutoa mchango wangu katika hii Wizara muhimu kama tunavyofahamu kwamba Wizara ya Kilimo ndiyo Wizara muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu wa mwaka 2016/2017 nilisimama kwenye Bunge hili, niliipongeza Serikali kupitia mfumo mzuri wa stakabadhi ghalani. Nilithubutu kusema kwamba mimi ni miongoni mwa waumini wa mfumo huu wa stakabadhi ghalani, ninaamini ni mfumo pekee ambao utaweza kumkomboa mkulima wa korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilieleza pia changamoto zilizopo kupitia mfumo huu wa stakabadhi ghalani. Mfumo huu wa stakabadhi ghalani, miongoni mwa changamoto zilizopo ni pamoja na wananchi kutokulipwa pesa zao kwa wakati. Waheshimiwa Wabunge wengi wamelizungumza jambo hili na katika vikao vilivyopita tulisema kwamba wananchi hawa wanapolima korosho na mazao mengine tumaini lao ni kutatua matatizo yao ikiwemo kusomesha watoto wao na mambo mengine mengi hata ikiwezekana kwa wale wababa ambao wanakusudia kuongeza wake wengine kupitia pesa hizi, lakini kinyume chake kimekuwa sivyo, wananchi wengi wamekuwa wakipata misukosuko. Sheria inaeleza kwamba baada ya kuuza korosho ndani ya siku saba mkulima anatakiwa apate pesa zake, lakini imekuwa sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi tunavyozungumza wapo wakulima ambao wanaendelea kudai pesa zao. Sisi Wilaya yetu ya Tunduru zaidi ya shilingi milioni 200 wakulima wanadai, inawezekana pengine kupitia udhaifu wa makarani waliopo katika vyama vyetu vya msingi na ninapozungumza makarani waliopo kwenye vyama vya msingi naamini kwamba taasisi hii inahusika moja kwa moja na ushirika, lakini inahusika moja kwa moja na Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napata shida sana kwenye jambo hili kwa sababu mara nyingi tumelizungumza hapa kuona umuhimu wa wananchi kupata pesa zao. Sasa niombe Waziri atakapofika atueleze ni lini sasa wananchi wale watapata hizi pesa kwa sababu tumewahamasisha waweze kuuza mazao yao kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani, lakini badala yake imekuwa matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kutolipwa pesa na wakati, liko jambo lingine ambalo limejitokeza, wananchi kupata malipo yao kupitia benki, sina uhakika kama ni jambo la kisheria. Ninaweza nikazungumza upande wa korosho lakini baharti nzuri wako Wabunge wengine wamezungumza hata kupitia mazao mengine. Inaonekana kama ni jambo la lazima kwamba wananchi wapate pesa zao kupitia benki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana Serikali ilikuwa na nia njema katika kuona fedha za wananchi zinabaki katika mikono salama, lakini badala yake imekuwa sivyo. Wakati wa mauzo ya korosho ukija Wilaya ambazo zinahusika na mazao haya utawahurumia wananchi. Wanapanga foleni kwenye mabenki, mtu anatoka kilometa 100 anakuja Makao Makuu ya Wilaya kufuata pesa yake, anakuja anaweza akakaa wiki nzima lakini anapofika dirishani anaambiwa pesa yako wewe haijaingizwa kwenye akaunti yako, mkulima yule anarudi kijijini, anarudi tena mjini imekuwa usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hilo basi tutofautishe kwa sababu siyo wakulima wote ambao wanapata mazao kwa kiwango kinachofanana, wako wakulima wengine wanauza mazao yao kwa uchache kadri ya Mwenyezi Mungu alivyomjalia kuvuna, sasa tunamtaka hata mtu wa kilo tano aende akapokelee pesa zake benki, mtu wa kilo 50 aende akapokelee pesa zake benki, mtu wa kilo 100 aende akapokelee pesa zake benki.

Mimi naomba kama ni jambo la kisheria basi ni vizuri tufanye marekebisho. Wananchi hawa wanakata tamaa na huu mfumo. Inafika mahali wanaona kwamba siyo mfumo mkombozi, kwa hiyo mimi niombe na nimuombe Mheshimiwa Waziri ni vizuri kama ni jambo la kisheria na sheria hiyo iwe imetungwa na Bunge hili walete tufanye mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwamba dhamira kubwa ya hawa wakulima wanapolima ni kutatua matatizo yao. Mtu ameuza korosho toka mwezi Novemba mpaka leo hajapata pesa yake, naliongea jambo hili kwa masikitiko makubwa na mimi ni sehemu ya wakulima wa korosho inauma sana, naomba Serikali ilitilie mkazo jambo hili katika kufanya marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie suala la viuatilifu ikiwemo mbolea na sulphur. Wabunge wengi wamezungumza kuhusiana na suala la upatikanaji wa mbolea, tumekuwa tukisema sana, mbolea hizi haziji kwa wakati lakini leo tumepunguza ruzuku. Ukija kwenye sulphur, mwaka jana mimi nilisimama hapa kuchangia wakati tunasema kwamba Serikali itatoa sulphur bure, tuliipongeza Serikali, lakini tuliwaomba ni vizuri muweke mfumo sahihi ambao utaelekeza ni namna gani wananchi hawa watapata sulphur bure, leo mmekuja na mabadiliko mengine, hivi kweli tuna nia ya kuliendeleza zao la korosho kama siyo nia ya kuliharibu zao la korosho? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilizungumze hili kwa sababu sote tumehamasika sasa hivi na ndiyo maana Waziri husika amefika mahali amepeleka miche ya korosho maeneo ambayo ana uhakika hata korosho hazitaota Wabunge wamesema hapa, ni kwa kuona korosho zimeongeza pato la Taifa letu, ni jambo jema lakini kwa nini tusisimamie tukaona hivi viuatilifu vinapatikana kwa wakati? Hii sulphur tumeeleza kwenye kitabu cha Waziri katika ukurasa wa 30 kwamba sulphur wanetegemea kwamba Bodi ya Korosho itatangaza bei. Hivi tunavyozungumza tayari korosho zimeanza kuchipua lakini mpaka leo bado…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kusimama katika Bunge hili na kupata fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi lakini nimpongezee Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote katika Wizara hii kwa kazi nzuri wanazofanya. Nimesikiliza vizuri hotuba ya Waziri jinsi gani wamejipanga kuhakikisha wanaweka miundombinu salama kwenye suala la elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze ukurasa wa 8 wa hotuba ya Waziri ambapo amezungumzia Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi. Katika ukurasa huo amezungumzia Chuo cha Mbinga na Chuo cha Nandembo kilicho katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru. Kama nitakuwa na kumbukumbu sahihi, Chuo kile cha Nandembo majengo yake yalijengwa mwaka 1947, majengo yale yalikuwa ya mission lakini yalikabidhiwa Serikalini kwa maana ya kuanzisha chuo mwaka 1978.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshawishika kusimama na kukiongelea chuo kile kulingana na mazingira magumu yalikuwepo pale. Waziri amesema kwamba anafikiria kutenga pesa kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu. Nimesimama kwa ajili ya kutaka kumkumbusha Mheshimiwa Waziri kwamba katika mwaka wa fedha 2017/2018 chuo kile walikitengea shilingi milioni 700 kama sijasahau kwa ajili ya kujenga karakana lakini mpaka leo nimesimama hapa pesa zile hazijanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kuanzisha vyuo hivi ni kwa sababu siku za nyuma shule za sekondari zilikuwa chache. Watoto wanapomaliza darasa la saba walikuwa wanapelekwa kwenye hivi vyuo kwa ajili ya kupata stadi mbalimbali za kazi ikiwepo useremala, ufundi magari, cherehani, mapishi na mambo mengine mbalimbali. Cha ajabu na ambacho kinachonisikitisha naona sana kipaumbele si kwa vile vyuo, hatuwasaidii watu wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia chuo hiki ambacho nakizungumzia majengo yake ni chakavu. Mheshimiwa Waziri siku za karibu alikuja Mkoa wa Ruvuma kwa ziara Mheshimiwa Rais lakini nimwombe aje rasmi atembelee Halmashauri zetu za Mkoa wa Ruvuma ikiwemo Halmsahuri ya Wilaya ya Tunduru ili ajionee mazingira yaliyopo. Katika chuo kile walimu wanaotakiwa ni 17 lakini tuna walimu watatu (3), hivi kweli tunakusudia kuwasaidia watoto kwenye lengo letu lile ambalo lilifikiriwa na Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tuna dhamira ya dhati ya kutaka kuwasaidia watoto wetu kupata stadi mbalimbali ni vizuri tukaona umuhimu wa kutenga hata hao walimu ili kuwapeleka kwenye maeneo haya waendelee kusaidia. Pia itapendeza zaidi kuweka miundombinu na kujenga hizo karakana ambazo zitasaidia sana wanafunzi ambao watakuwa katika shule hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala ambalo wenzangu wamelizungumza la watumishi mbalimbali katika Wizara hii na hususani walimu. Nimeona hivi karibu Mheshimiwa Waziri Jafo akisema kwamba wameajiri walimu na amesisitiza walimu wale waende katika shule zile ambazo wamepangiwa. Sina hakika kama wameangalia matatizo yaliyopo kule. Kama kweli wameangalia matatizo yalipo kule sina shida lakini wamezungumza Wabunge wenzangu kuhusiana na suala la walimu na mimi naomba nisisitize kwamba mpaka hivi tunavyozungumza kwenye shule zetu walimu ni wachache, kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaongeza spidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kwanza kabla ya kuangalia wale walimu ambao walikuwa na vyeti feki na walimu hewa lakini siku za nyuma pia tulikuwa na upungufu wa walimu, kwa hiyo, tuna mapengo hayo ya kuhakikisha tunayaziba. Kwa hiyo, niiombe hii Serikali ya Chama cha Mapinduzi, Serikali sikivu kupitia Waziri, Mheshimiwa Profesa Ndalichako hakikisheni jambo hili la kuajiri walimu linapewa kipaumbele. Hata sisi tulioko humu ndani kama siyo walimu tusingeweza kufika hapa. Kwa hiyo, jambo hili ni jema katika kuhakisha tunapanga walimu katika shule zile. Ukienda kwenye shule nyingine inasikitisha, shule inatakiwa walimu 10, 15 unaweza ukakuta walimu 2, hatuwasaidii watoto. Kwa hiyo, naomba sana tuzingatie hilo kupitia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie suala nyumba za walimu, wenzangu pia wamesema na mimi naomba niseme walimu wetu walio wengi wanaishi katika mazingira magumu sana. Mazingira pia ya kufundishia yanashawishi pia mwalimu kuwa mzuri katika eneo analofanyia kazi. Niombe sana Mheshimiwa Prof. Ndalichako suala la nyumba za walimu na madarasa lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Ruvuma, sina hakika ns maeneo mengine lakini mpaka hivi ukienda unaweza ukakuta madarasa ambayo yameezekwa kwa nyansi. Ndiyo maana nimemuomba Mheshimiwa Waziri akimaliza bajeti hii afike kule aone hali halisi ili haya tunayozungumza Waheshimwa Wabunge kupitia vikao hivi basi hata yeye ataenda kuona uhalisia. Darasa moja watoto wa darasa la tano wanaangalia ubao upande mwingine, watoto wa darasa la sita wanaangalia upande mwingine. Unaweza ukaona ni kitu cha ajabu lakini hivyo vitu vipo katika maeneo yetu mpaka hapa tunapozungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni jukumu la Serikali kuhakikisha tunaondoa hizo changamoto. Yapo mambo mengi mazuri yanafanyika lakini palipo na mambo mengi mzuri lazima kuna changamoto na changamoto lazima kuzibaini na kuzitafutia ufumbuzi wake. Mheshimwa Waziri hali za elimu kule ni ngumu, nasisitiza sana mama yangu mpendwa uje mkoani uone si tu ukikaa pale ukitembelea Kigoma unakuta umemaliza mkoa njoo na Ruvuma uone hali ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Wakaguzi wa Shule. Suala hili Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamelisema na mimi naomba nisisitize jambo hili. Wakaguzi hawa wa Shule wana mazingira magumu. Kwenye Halmashauri zetu sisi Wabunge ni Madiwani unaona jinsi gani Wakaguzi hawaendi kwa mujibu wa ratiba kutembelea zile shule na kuangalia mwenendo mzuri wa elimu yetu. Nikuombe ipo haja sasa ya kuhakisha Wakaguzi wanapatiwa magari, mafuta na wanawezeshwa kwa namna moja au nyingine ili wafike kwenye maeneo mbalimbali ili tupokee taarifa zilizo sahihi vinginevyo tunaendelea kupokea taarifa zinazopikwa kila mwaka kwa sababu hawana uwezo wa kufika kwenye maeneo yale. Nalisisitiza hili naamini kabisa ni sehemu ya kuboresha elimu yetu, elimu ya msingi pia ya sekondari, nasisitiza sana Wakaguzi wana hali ngumu katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la kupandishwa vyeo walimu, nina hakika ni haki ya mtumishi kwamba anapostahili apate lakini wengi wamekuwa wakilalamika na hawapati fursa hizo. Nimwombe Mheshimiwa Waziri toa maagizo katika maeneo yanayohusika inapofika wakati mwalimu anastahili kupandishwa daraja, apandishwe kwa sababu ni haki yake. Katika maeneo mengine walimu wamekuwa wakilalamika kwamba anatakiwa kupandishwa daraja lakini hapandishwi, tunawakatisha tamaa walimu wetu kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la uhamisho wa walimu. Naamini Wizara hii inategemeana na Wizara ya TAMISEMI. Tunalo tatizo, walimu wengine na hasa maeneo ya vijijini wanakaa kule kana kwamba ni adhabu. Mwalimu anamfundisha mama mtu, mtoto mtu, mjukuu mpaka anazeeka kwenye shule ile ile. Inafika mahali inaonekana kama kuna upendeleo fulani katika uhamisho wa walimu. Niombe tuzingatie na tuwaangalie wale walioko vijijini, tutoe motisha kwa walimu wetu ili waendelee kufanya vizuri. Inapoonekana kwamba nay eye anatakiwa apate uhamisho basi ni vizuri ahamishwe aende maeneo mengine lakini anakaa anamfundisha mama/baba mtu, mtoto mpaka mjukuu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga nkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote na mimi napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kusimama hapa na kuendelea kuchangia kupitia Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na viongozi wote katika hii Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasema yale ambayo nakusudia kusema kupitia Wizara hii, naomba nieleze kwamba mimi ni Mjumbe katika Kamati hii. Nachofahamu mimi ni kwamba tumekuwa tukifanya kazi kupitia Kamati mbalimbali, naamini tunakuwa na Mwenyekiti wa Kamati ambaye anamwakilisha Mheshimiwa Spika lakini kunakuwa na Wajumbe kwenye Kamati zile mbalimbali ambapo tunakuwa tunawawakilisha Waheshimiwa Wabunge wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kupitia maneno ya utangulizi ambayo nimeyasema, naomba nieleze masikitiko yangu. Sisi kupitia Kamati yetu tumekuwa tukijadili mambo mengi mbalimbali na kuweka maazimio tukiwa tunaamini kwamba tunapoleta kwenye kikao hiki cha Bunge basi yanapata baraka, pengine kunatolewa ushauri kwenye maazimio hayo ili Serikali ifanye utekelezaji. Kinachoshangaza tumekuwa tukijadili mambo mengi, tunafanya maazimio lakini utekelezaji unakuwa wa kusuasua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye ule ukurasa wa 18 tumetoa maoni mbalimbali ya Kamati. Naomba niseme machache kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia. Jambo la kwanza ninalolisema ni kuhusiana na suala la kutenga pesa kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Tumelisema sana na tumekuwa tukitolea maazimio na kuleta mbele ya Bunge lakini jambo hili limeonekana ni sugu na halitekelezeki. Pesa hazipelekwi kwa wakati na pengine zinapelekwa kwa asilimia ndogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza suala la maji, sote tunafahamu kwamba maji ndiyo uhai na maji ndiyo kila kitu. Sisi kama Kamati tunaleta mbele ya Bunge lako Tukufu ili Waheshimiwa Wabunge wenzetu watoe maoni yao na bahati nzuri Bunge limekuwa likipitisha maazimio lakini tatizo ni kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatutapeleka pesa za miradi ya maendeleo kwa wakati hatuwezi kuwasaidia wananchi wetu. Haya yote tunayoyafanya itakuwa sawasawa na hakuna kitu chochote kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, sisi kupitia Kamati yetu tuliazimia na tulileta kwenye Bunge Tukufu, lakini kabla ya Bunge lilipelekwa kwenye Kamati ya Uongozi, nafikiri huo ndiyo utaratibu, kuhusiana na suala la kuongeza shilingi 50 katika Mfuko wa Maji. Wabunge wengi wamesema na mimi naomba niseme kwa masikitiko makubwa sana. Sielewi tatizo linakuwa wapi kwa sababu sisi tunasema kulingana na matatizo tuliyokuwa nayo kwenye maeneo yetu na tulishawishika kusema hivi tukifikiri kwamba inawezekana lakini tukija hapa inakuwa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Waziri atakapokuja leo atuambie kwa sababu jambo hili sisi tulianza kuzungumza kwenye Kamati kwa nguvu sana, Wabunge tulisema sana. Bahati nzuri hili sio Bunge la kwanza kujadili jambo hili, kama sijasahau kuna Mabunge kama matatu tumekuja tunapitisha maazimio lakini wanapokuja kwenye Serikali wanapokwenda kwenye Kamati ya Bajeti majibu yanakuja sivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukuombe kwamba hili jambo sasa wakati umefika wa kutekelezwa. Hiki kiasi ambacho sisi kama Kamati tulipendekeza lakini kupitia Bunge pia wenzetu waliunga mkono na tulifanya maazimio, tatizo ni nini? Tunaomba tutekeleze, tutenge hizi pesa kwa ajili ya kutunisha kwenye ule Mfuko wa Maji ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu. Kama sivyo tuombe safari hii tuambiwe na Serikali njia nyingine, kama tunaona shilingi 50 haitoshi basi watuambie mbadala wake ili sisi tupitishe maazimio kwa sababu wetu wana shida ya maji. Kama mnaona hiki sio chanzo stahiki basi tuleteeni chanzo kingine ili sisi tupitishe maazimio wananchi wetu wapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona niyaseme haya na nimetanguliza kusema kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati, toka tumeingia kwenye Kamati ile katika mambo ambayo tunayazungumza ni kuona ni namna gani tunapata maji. Waheshimiwa Wabunge wenzetu sisi tunaomba hili mtuunge mkono kwa sababu tukiwa kwenye Kamati tunafanya kazi kwa niaba yenu ninyi na tunapoleta hapa tunaomba tufanye maazimio ili utekelezaji ufanyike. Sasa Waziri utakapokuja utatuambia tatizo liko wapi na kama siyo shilingi 50 basi tuambie ni nini kitakuwa chanzo ili wananchi wetu wapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeanza kuyasema hayo maazimio ya Kamati ambayo tumekuwa tukiyasema na tunayaleta kwenye vikao na bahati nzuri Kamati hii mara nyingi inaleta kwenye Bunge lako mambo ambayo na wenzetu wanayakubali. Niombe tu Waziri aseme hili jambo tunalitekeleza kwa utaratibu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida ya maji ni kubwa sana na mimi ni sehemu ya akina mama na nafahamu jinsi gani akina mama wenzangu wanapata shida katika suala la maji. Tunayo maeneo mengi katika nchi yetu yana tatizo la maji, maji ni ya shida sana. Sisi tuliopo humu ndani bila maji hata hizi suti zisingekuwepo, tusingependeza; hata mitandio tunayoivaa isingeng’aa bila maji lakini hata kuoga nako kunahitaji maji, kama hakuna maji ni mtihani mkubwa sana, hili ni jambo kubwa sana. Tuombe Waziri atakapokuja aseme neno kupitia Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nami napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kusimama katika Bunge lako hili na kupata fursa ya kuchangia taarifa mbalimbali kutoka kwenye Kamati ambazo zimewasilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuingia Bungeni, Kamati yangu ya kwanza ilikuwa Kamati ya UKIMWI, lakini baadaye nilienda kuwa Mjumbe katika Huduma za Maendeleo ya Jamii. Kwa hiyo, mimi ni kama Mjumbe Mstaafu kwenye hizo Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupongeza sana sana kwa kazi nzuri ambazo zinafanyika. Nimeanza kusema kwamba nilikuwa Mjumbe kwenye hizi Kamati, niliona kule mwanzo jinsi tulivyokuwa tunapata shida kwenye baadhi ya mambo, lakini naona baada ya kupitia taarifa hizi, kwa kweli kwa sasa yako maeneo ambayo tunafanya vizuri sana, sina budi kupongeza kwa Wenyeviti wa Kamati, Wajumbe wa Kamati na hata Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la ujenzi wa Vituo vya Afya. Binafsi naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazofanya. Wako Wajumbe wamesema tuna tabia ya kupongeza sana halafu baadaye tunalaumu sana. Kama binadamu, kunapokuwa na jambo zuri ni lazima usime, lakini hakuna mazuri yasiyekuwa na changamoto. Tunaeleza changamoto kwa ajili ya kuishauri Serikali ili iendelee kufanya vizuri vile ambavyo imekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kama mwanamke, lakini siyo tu mwanamke, ni mwanamke ambaye nimeshawahi kuingia leba, nimeona matatizo ambayo tumekumbana nayo huko nyuma kupita maeneo ya uzazi na leo jinsi mambo yanavyokwenda vizuri. Kwa kweli naomba nipongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Serikali imeweza kujenga Vituo vya Afya 350. Katika Vituo vya Afya hivyo, katika Mkoa wangu wa Ruvuma tumepata Vituo vya Afya saba. Vituo hivyo saba ni pamoja na vilivyopo katika Wilaya ya Tunduru, Kituo cha Afya Matemanga, Mkasale na Mchoteka. Ninashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie Kituo cha Afya Matemanga ambacho kwa sasa tayari kimeanza kutoa huduma ya upasuaji, nafikiri ndiyo lengo la Serikali kukaribisha huduma ili akina mama wanapopata dharura ya upasuaji, waweze kupata hiyo huduma kwa haraka sana. Naomba sana niipongeze Serikali kwa hiki ninachokisema.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawapongeza viongozi ambao wameshiriki kwa namna moja au nyingine, akiwepo Diwani wa Kata ile ya Matemanga; amejitahidi sana kufuatilia kwa Serikali, amepiga kelele na hatimaye tumefanikwa, tuna uwezo sasa katika kituo kile kufanya upasuaji wa akina mama wajawazito. Vile vile wanapasuliwa akina baba wenye matatizo ya ngiri na huduma nyingine. Kwa kweli nawapongeza sana na ninawatakia kila heri kwa namna moja au nyingine wale ambao wamehusika katika kufanikisha zoezi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba nizungumze suala la mikopo ya asilimia 10. Ni kweli kupitia Halmashauri zetu na kupitia mapato ya ndani, zipo Halmashauri ambao zinafanya vizuri lakini zipo ambazo mpaka sasa bado zinatekeleza jambo hili kwa kusuasua. Naomba nitumie nafasi hii kupongeza Halmashauri ambazo zinafanya vizuri kupitia hii asilimia 10
kwa lengo la kukopesha akina mama, vijana na walemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukiwasaidia akina mama wajasiriamali wadogo wadogo kuweza kuinua mitaji yao. Kwa kweli jambo hili ni jema. Naiomba Serikali, kwa zile Halmashauri ambazo hazitekelezi vile ambavyo inakusudiwa, ni lazima kuchukua hatua kuona kwamba kila Halmashauri inatekeleza ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo la walemavu. Katika kutekeleza hili jambo kuna miongozo ambayo inatolewa na Wizara, wanapeleka kwenye Halmshauri kwa ajili ya kuziagiza Halmashauri zitoe pesa kwa kufuata miongozo hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kwenye suala la walemavu. Naomba niishauri Serikali kwenye suala la walemavu ambalo lina shida kidogo. Katika kupitia ile miongozo, inawataka pia walemavu nao wapate ile mikopo kupitia vikundi vya watu watano watano. Ninaamini kabisa kwamba tunapozungumza vikundi, viwe ni vya watu walioshibana ili waweze kuchukua mkopo na kulipa, lakini yapo maeneo mengine walemavu wanashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kupitia maelekezo yanayotolewa, lingetolewa kabisa eneo maalum la kumtaka hata mlemavu mmoja mmoja aweze kupata mikopo. Kwa sababu maeneo mengine wanashindwa. Unaweza kwenda kwenye kijiji pengine wanatakiwa watano watano, lakini wakakosekana idadi inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana kupitia Serikali yangu na sina shaka ni Serikali sikivu; kwa kuwa tuna lengo la kuwasidia walemavu, basi kuna vitu ambavyo tunatakiwa tuviangalie upya ili tulegeze masharti tuweze kuwasaidia, tuhakikishe na wale walemavu wananufaika na hii huduma na mikopo ili iweze kuwaendeleza katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambao naomba nilizungumze ni suala la ikama ya watumishi. Tunafahamu kwamba tuna tatizo la ikama ya watumishi katika idara mbalimbali, lakini naomba nizungumze kwenye suala la Maafisa Maendeleo ya Jamii wa ngazi ya Kata. Kwenye Halmashauri zangu nane zilizopo katika Mkoa wa Ruvuma, naomba nitolee mfano kwenye Halmashauri moja ambao wana uhitaji wa Maafisa wa Maendeleo ya Jamii 39, lakini mpaka sasa wapo 13. Hata wale 13, wengine wamepelekwa kwenye Idara nyingine kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Maafisa Maendeleo ya Jamii wana kazi kubwa sana. Kazi mojawapo ni kuhakikisha miradi ile ya maendeleo inayokwenda kwenye maeneo wanatoa ushauri mbalimbali. Hata hii mikopo tunayozungumza, Maafisa Maendeleo ya Jamii wa ngazi ya Kata ndio wanaotakiwa waifanye hii kazi ya kuleta uhamasishaji kwa vikundi hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hii mikopo inanapotolewa wakati mwingine, vikundi vingine vinashindwa, vinasuasua katika kufanya marejesho; na dhamira ya Serikali itoe mikopo na hatimaye watu weweze kurejesha mikopo. Kwa hiyo, wenye kuweza kuleta hamasa ni wale Maafisa Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri hivi karibuni Mheshimiwa Waziri wa Utumishi alitembelea katika Halmashauri yetu, aliona mazingira yaliyopo kuhusiana na suala la watumishi. Naomba sana nisisitize kwenye eneo hili kwamba watumishi waliopo ni wachache. Unaweza ukaona na pia Wizara husika inaweza ikaona. Kama wanatakiwa 39 halafu unakuta kuna 13, lakini bado hata 13 wenyewe wameenda katika Idara nyingine katika kusaidia kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niipongeze sana Serikali yangu na Wizara kwa kazi nzuri inayofanyika. Tunawatakia kila heri, wafanye kazi vizuri ili CCM iendelee kushinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante niungane na wenzangu kupongeza Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. Pamoja na pongezi hizo naomba niende moja kwa moja katika mambo ambayo nakusudia kuyachangia. Nakusudia kuchangia mambo yafuatayo; kwanza kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukianzia ukurasa ule wa 29 mpaka 32 wamezungumzia kuhusiana na suala la zao la korosho. Na zao la korosho katika maeneo yafuatayo;

Mheshimiwa Spika, kwenye ule ukurasa wamezungumzia suala la uzalishaji wa miche ambalo lilifanyika katika msimu wa 2017/2018. Ninachokumbuka kwamba kupitia Bodi ya Korosho walitoa maelekezo kwa halmashauri ili waandae vikundi wazalishe miche ile ya korosho na wote tutakuwa mashahidi miche ambayo ilizalishwa ilipelekwa katika maeneo mengi katika na wameeleza ni mikoa 17 ambayo ilipelekwa miche ile.

Mheshimiwa Spika, mpaka hivi ninavyosimama hapa wako wanavikundi ambao waliingia mikataba na Bodi ya Korosho hawajalipwa pesa zao niombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja alizungumze hili kuona namna gani kwa sababu tunapozungumzia wanavikundi tunagusa jamii zetu na ni watu ambao wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu sasa walifanya hii kazi lakini mpaka leo unapozungumza hawajalipwa. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja kutoa ufafanuzi tueleze ni kwa nini hawajalipwa na vinginevyo nitashika shilingi kwa mara ya kwanza nakusudia kushika shilingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo nakusudia kuzungumza ni suala la ujenzi wa maghara, nafahamu kwamba yako maeneo ambayo tulikuwa tunaendelea kujenga maghara napozungumza maghara ni yale maghara ambayo tunafikiria kwa ajili ya uhifadhi wa korosho. Kuna Mkuranga na kuna Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru na tayari ujenzi huuulianza lakini ninapozungumza sasa hivi ujenzi huo umesimama, niombe Mheshimiwa Waziri atueleze tutamaliza lini yale majengo.

Mheshimiwa Spika, nimeshawishika kulisema hili kwa sababu hivi tunavyoendelea tunaingia katika mfumo wa ununuzi wa Ufuta na tu na tunapozungumza sasa korosho nyingi ziko maghalani, sasa sijui itakuwaje kwenye hili jambo kwamba Ufuta unatakiwa uingie kwenye maghala lakini maghala yamejaa korosho mpaka korosho hazijaondolewa, kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja pia utuambie ule ujenzi utakamilika lini, kwa sababu tulipanga sisi kupitia Serikali yetu lakini bado hatujakamilisha ujenzi wa maghala likiwemo ghala lile katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru lilitengewa pesa ilitoka pesa kidogo na sasa ujenzi umesimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine naomba nizungumze suala la Maafisa Ugani, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamelisema lakini pia naomba niliseme tunazungumza kulima kilimo cha kisasa. Naomba niseme kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu wako wakulima wetu mpaka hivi tunavyozungumza hawajui hata namna ya matumizi ya hizi pembejeo sasa ili waweze kutumia pembejeo ni pamoja na kuwepo Maafisa Ugani katika vijiji vyetu ili waendelee kuwaekeleza wakulima wetu katika kulima kilimo bora na chenye ufanisi.

Mheshimiwa Spika, nimelazimika kushawishika kuyasema haya kwa sababu ni miongoni mwa Wabunge wanaotoka katika Mkoa wa Ruvuma na sisi Ruvuma ina wakulima tunalima kilimo cha chakula, lakini pia tunalima kilimo cha biashara ili tuwasaidie wananchi wetu ni pamoja na kuwapeleka Maafisa Ugani na hii ni sera kabisa lazima wawepo Maafisa Ugani, kwa hiyo suala la Maafisa Ugani kwanza ikumbukwe tunao wachache lakini hata wale tuliokuwa nao hawafanyi kazi ipasavyo, wengine wanageuka kuwa wanasiasa, lakini kuna sintofahamu katika ya Afisa Ugani anayeshughulika na masuala ya uvuvi na anayeshughulika na masuala ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kwenye vijiji vyetu akimuono Afisa Ugani anayehusika na masuala uya uvuvi ana amini kwamba anaelewa na masuala ya kilimo, sasa niombe kupitia hii Wizara na masuala ya mifugo niombe kupitia Wizara tuone uwezekano wa kuwapeleka Maafisa Ugani ili waendelee kuwasaidia wakulima wetu. (Makofi)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Sikudhani.

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante naunga mkono hoja mambo ni mengi lakini muda mchache ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia kusimama katika Bunge lako hili ninaamini hii ni bajeti ya tano na kwa lugha nyingine ni bajeti ya mwisho kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu wenzangu wengi wamempongeza Mheshimiwa Rais na wamesema sababu mbalimbali. Lakini naamini kwamba ili awe Rais lazima kuna michakato ilianza mchakato wa kwanza Rais alitokana na Chama cha Mapinduzi. Mwaka 2015 Mheshimiwa Rais alikabidhiwa Ilani kutoka kwenye Chama chake cha Mapinduzi, Ilani ambayo ilikuwa imeainisha mambo mbalimbali ambayo yatatekelezwa katika kipindi hiki cha miaka mitano. Naomba niseme kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu nampongeza kwa dhati Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi ya yote Mheshimiwa Rais ni binadamu kama binadamu wengine anapofanya vizuri ni lazima tumpongeze na kumpongeza ni kumtia moyo ili aendelee kufanya vizuri naomba niungane na wote ambao wanampongeza tulioko ndani ya Bunge lakini na wale walioko nje ya Bunge kwa sababu sote tunaona kazi nzuri ambayo inafanyika na Mheshimiwa Rais hakika tunampongeza na tunaendelea kumuombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kuwatumikia wananchi katika taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nikupongeze wewe ambaye leo umekalia kiti lakini ninaamini kabla ya wewe yupo Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hii taasisi ambayo umeisimamia ni taasisi kubwa sana mmetusimamia watu wengi wenye tabia tofauti tumekuwa tukiona katika taasisi zingine mbalimbali watu hawamalizi wakiwa wamoja lakini naendelea kuamini kwamba tunamaliza Bunge tukiwa wamoja hongereni sana na In Shaa Allah Mwenyezi Mungu aendelee kuwaweka ili mushike nafasi hizo katika kipindi kijacho. Ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme mambo machache kupitia Wizara hii ya TAMISEMI nafahamu kwamba tunajadili mapato na matumizi katika Wizara hii ya TAMISEMI lakini kabla sijasema yale ambayo nayakusudiwa pia naomba nimpongeze kaka yangu Jafo. Watu wamemsema kwa sifa mbalimbali. Naomba niseme sifa moja miongoni mwa sifa alizokuwa nazo Mheshimiwa Jafo ni msikivu hana unyanyapaa kwa Wabunge wenzake ukitoka ukienda kumpelekea hoja yako anakusikiliza na amekuwa akitusaidia katika kutekeleza mambo mbalimbali katika Majimbo yetu nakuombea kaka yangu endelea kufanya vizuri na In Shaa Allah wananchi katika Jimbo lako watakuona utarudi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la mikopo ya 10% nafahamu kwamba tunazungumza mikopo ya 10% ni pesa ambazo zinatokana na mapato ya ndani katika halmashauri zetu. Hizi 10% tumezitenga katika maeneo matatu 4% vijana, 4% wakinamama na 2% ya walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo naomba niseme katika eneo la walemavu mikopo hii inatolewa kwa kuunda vikundi mbalimbali sasa nilikuwa naomba nishauri kupitia Wizara hii kwamba katika uundaji na utoaji wa mikopo hii ya 2% kwa upande wa walemavu, ziko changamoto zingine ambazo zinajitokeza katika utekelezaji inawezekana kabisa walemavu wapo katika maeneo mbalimbali unaweza ukakuta kijiji kimoja kina mlemavu lakini kijiji X hakina mlemavu ndani ya kata lakini sifa mojawapo ya hawa walemavu kupata mikopo ni kujiunga katika vikundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba jambo hili liangaliwe kwasababu tumeweka jambo hili mahususi kwa upande wa walemavu ikiwezekana wakopeshwe hata mlemavu mmoja mmoja siyo lazima wakopeshwe kupitia vikundi. Nafahamu kwamba wanapounda kikundi mara nyingi kinatakiwa kikundi cha watu wanaoaminiana sasa huwezi kutoka kwenye kijiji X ukaenda kumpata kwenye kijiji B mlemavu mwingine ili muungane watu ambao hamfahamiani inakuwa haipendezi na kwa namna nyingine inaweka ugumu katika kuwasaidia hawa walemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana sana tuwaangalie sana katika kuwasaidia hawa walemavu kulingana na ile dhamira ya Serikali tupunguze masharti kwa upande wa walemavu. Ikionekana kwamba kuna mlemavu ambaye yuko kwenye kijiji X amekidhi vigezo vya kukopeshwa bila kujali yuko katika kikundi basi ni vizuri Serikali ikamuangalia na nafahamu hili Mheshimiwa Jafo analiweza kwasababu liko ndani ya utekelezaji wake tuendelee kuzishauri halmashauri zetu ili na wale walemavu waweze kupata hii mikopo bila kuwa na masharti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hivyo kwa sababu mwisho wa siku wakipata mikopo wanatakiwa warudishe sasa kama hawatakuwa watu wanaoaminiana inakuwa ngumu katika kuwafuatilia. Naomba nilisisitize hilo kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu tuwasaidie walemavu kwa kupunguza masharti kama nilivyosema Mheshimiwa kaka Jafo unaliweza liko ndani ya uwezo wako. (Makofi)

Jambo lingine naomba nipongeze Serikali kwa suala la ukarabati wa vituo vya afya. Vimeelezwa hapa vituo vya afya 433 ninaamini ni miongoni mwa vituo ambavyo vipo katika mkoa wangu wa Ruvuma, tumekarabati baadhi ya vituo vya afya na nafahamu kwamba lengo la kukarabati vituo vya afya ni kuweka huduma karibu kwa wananchi na sote tunafahamu tulikotoka ilikuwa siyo rahisi kuona kwamba kituo cha afya kinaweza kutoa hata huduma ya upasuaji kwa mama mjamzito. Lakini kwa vituo hivi vya afya ambavyo kwa sasa vinakarabatiwa vina lengo la kuokoa maisha ya akinamama wajawazito na watoto. Nasema hongera sana kwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine pia naomba nizungumzie kwenye suala la ukamilishaji baadhi ya zahanati kaka Jafo umesema kwenye taarifa yako kwamba ni milioni 150 katika kila halmashauri nafahamu ziko halmashauri mpaka ziko zahanati mpaka leo hatujafanya vizuri na kuna maboma, kwa hiyo, ni vizuri tukaziangalia zile zahanati ambazo tayari tulishaanza kuzikarabati lakini zimesimama kwa ukosefu wa pesa, kwa hiyo, pesa hizi zielekeze kwenye kukarabati katika zile zahanati ambazo tayari Serikali ilishapeleka pesa lakini zimesimama kwa ajili ya kukosa pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nimeona mambo mbalimbali ambayo yanaendelea katika mkoa wangu ikiwemo ujenzi wa hospitali katika Jimbo la Madaba ambapo bilioni 1 imetengwa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali. Naona umewasha taa naomba nimalizie suala dogo tu kwa ridhaa yako na unafahamu kwamba katika uchangiaji huu mimi ni mtoto wa mwisho. Kwa hiyo, naomba na mtoto wa mwisho anahitaji kuvumiliwa naomba univumilie kama dakika tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala moja suala la milioni 140 kukamilisha maboma katika shule za msingi nasema niliseme hili kwa sababu nafahamu yako maboma mengi yamejengwa kwa nguvu za wananchi, wananchi walifyatua tofali wananchi walisomba mchanga wananchi walikusanya mawe lakini maboma yale hayajakamilika naishukuru sana Serikali niombe pesa hizi ziende zikafanye kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunivumilia naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi, wa Mwaka 2016
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema na kuwepo katika kikao cha leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi kwanza napenda niipongeze Serikali yangu na Wizara husika kwa kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania 2016. Kwa nini nalazimika kuipongeza Serikali na Wizara? Ni kwa sababu nafahamu Muswada huu unalenga kuendeleza, kuongeza na kuboresha uelewa wa wakulima wetu Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Muswada huu yamezungumzwa mambo mengi katika kufanya utafiti. Naomba nijikite kwenye suala la utafiti wa mbegu bora. Waheshimiwa Wabunge wengi jana wakati wanachangia wameeleza sana uwepo na mbegu bora za mazao ya chakula na biashara. Mimi mwenyewe nimewahi kutumia mbegu za mahindi ambazo zinaletwa na haya mashirika mbalimbali, cha kushangaza nilipanda kama heka 10 lakini shamba lote mahindi hayakuota.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inawezekana jambo hili lilinigusa mimi lakini pia liliwagusa wakulima wetu, mambo kama haya kwa kweli yanakatisha tamaa. Kwa hiyo, binafsi naamini kwa kupitia taasisi hii ambayo itafanya utafiti tutakuwa na mbegu bora. Miongoni mwa vitu ambavyo mimi binafsi nasisitiza ni kupatikana kwa mbegu bora ambazo hazitakatisha tamaa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutokuwa na mbegu bora maana yake tunawafanya wananchi wetu waendelee kutunza mbegu zile kwa teknolojia ambazo zimepitwa na wakati labda kwa kufutika mbegu kwenye moshi ili mwaka mwingine ikasaidie. Kwa karne hii ambayo tunakwenda nayo binafsi naona sio jambo jema. Kwa hiyo, nasisitiza sana katika eneo hili la utafiti tuzingatie upatikanaji wa mbegu bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na jambo hilo pia naomba nisisitize suala la uhifadhi wa mazao. Wakulima watalima mashamba, watapanda mbegu na hatimaye watavuna. Katika eneo hili, wakati wakulima wetu wa mazao ya biashara na chakula wanasubiri soko mara nyingi Serikali imekuwa ikiwasisitiza wasiuze mazao yao. Katika kipindi kile ni wajibu wetu sasa kuwaelimisha njia bora ya uhifadhi wa mazao ili viwango na ladha ile isipotee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi yetu nimeshuhudia tumekuwa tukiunda Bodi mbalimbali lakini mara nyingi hatuzisimamii. Mfano mzuri ni Bodi ya Korosho. Hivi karibuni tumefanya kikao cha wadau wa korosho Bagamoyo, kwa bahati nzuri Waziri mwenye dhamana alikuwa mgeni rasmi katika kikao kile, alizungumzia masuala mengi na changamoto zilizopo kwenye Bodi na Mfuko ule wa Wakfu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mwenyekiti wa Bodi amepata fursa ya kujibu maelezo ambayo mgeni rasmi aliyaeleza, alimwomba Waziri kwamba siyo vizuri kusubiri mikutano ya wadau, ni vizuri Wizara iwe inashirikiana moja kwa moja na Bodi katika kutatua changamoto zilizopo na kutoa ushauri. Kwa hiyo, nasisitiza katika jambo hili kwamba tunapounda hizi Bodi ni wajibu wetu kuzisimamia ili kubaini changamoto zilizopo na kuzitatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Muswada huu pia tumezungumzia masuala ya uundaji wa Bodi na upatikanaji wa Wajumbe. Kwenye ile Bodi tumezungumzia upatikanaji wa wakulima kuwa wawakilishi kwenye Bodi. Kamati imependekeza kwamba kuwepo na wakulima wawili badala ya mkulima mmoja kama ulivyopendekeza Muswada. Hata hivyo, dada yangu Mheshimiwa Sakaya wakati analijadili hili na mimi binafsi nilipenda sana mchango wake alizungumzia kuhusu hizi Bodi na alifika mbali, alipendekeza kwamba Bodi hizi ni vizuri zikaenda Kikanda. Binafsi nilishawishika lakini baadaye nilipata shida nikasema tunaweza tukafika mahali tukaweka kikanda lakini kila kanda ina mazao mchanganyiko hatma yake tunaweza tukafika mahali sasa kila mwakilishi wa zao aingie kwenye Bodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nikubaliane moja kwa moja na mapendekezo ya Kamati kuwa badala ya yule mjumbe mmoja aliyependekezwa kwenye Muswada basi kuwepo na wajumbe wawili wakulima ambao wataingia kwenye hii Bodi. Sote tunafahamu kwamba kidole kimoja hakivunji chawa kwa kuingia wakulima wawili kutasaidia kutatua changamoto zilizopo. Hata hivyo, kubwa zaidi naomba tuangalie sifa za wale wakulima ambao wata…

MWENYEKITI: Ahsante.