Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Munira Mustafa Khatib (7 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia bajeti hii. Naomba kwanza nimshukuru Waziri wa Fedha na timu yake yote kwa kutuletea bajeti ambayo inaweza kwenda kumkomboa maskini wa chini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Serikali ina nia njema ya kumkomboa mwanamke mwenye kipato cha chini. Hata hivyo, cha kusikitisha vijana ambao ni zaidi ya asilimia 60 wamepatiwa shilingi bilioni tano kwa ajili ya kuendeleza ujuzi. Hii fedha ni kidogo sana kwa sababu vijana wanao-graduate kila mwaka ni zaidi ya 8,000. Kwa hiyo, naiomba Serikali iongeze pesa hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kweli tunaka kwenda kwenye nchi ya uchumi wa viwanda basi naomba Serikali iwe tayari kwenda kwenye nchi ya viwanda. Kivipi iwe tayari kwenda kwenye nchi ya viwanda? Ni kwa kuvilinda viwanda vyetu vya ndani kwani bado viwanda vyetu vya ndani Serikali haiko tayari kuvilinda.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Kiwanda hiki cha Urafiki ambacho Serikali inamiliki asilimia 49 lakini hawa wenzetu Wachina wana asilimia 50. Kiwanda hiki kinamilikiwa na Wachina si Serikali. Ukiangalia hapa kuna tofauti ya asilimia mbili tu ili Serikali kuweza kukimiliki lakini ndani ya bajeti hii ya 2016/2017 bado Serikali haijatenga fedha hii kwa ajili ya kukikwamua kiwanda hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Meneja ni kutoka China hajui vision wala mission ya Kiwanda hiki cha Urafiki. Hivi kweli tunatengenezaje ajira kupitia viwanda? Hivi ni vipi tunaweza kuwakomboa vijana wa Tanzania kwa kupata ajira? Kama hatuko tayari tungetafuta njia nyingine ya kusaidia vijana lakini si kwa njia hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna Kiwanda cha TANELEC ambacho kiko Jijini Arusha kinazalisha jenereta. Jambo la kusikitisha Serikali inaagiza transformer nje badala ya kununua kutoka kwenye kiwanda hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kweli tungekuwa tayari kununua transformer katika kiwanda hiki basi tungepata ajira nyingi kwa vijana na tungeweza kupata fedha kwa ajili ya Serikali yetu. Leo wanatoka watu nje ya nchi kuja kununua jenereta katika kiwanda hiki cha TANELEC lakini sisi Watanzania tunaagiza bidhaa kutoka nje ya nchi. Nina imani bado Serikali haijaamua kuinua uchumi wa viwanda Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la asilimia 5 ambazo kila Halmashauri inatakiwa itoe kwa ajili ya kusaidia wanawake na vijana. Kama kweli tuko tayari kumsaidia kijana, kama kweli tuko tayari kumsaidia mwanamke basi naiomba Serikali iweze kuleta fedha hizi kwa wakati. Naiomba Serikali iweze kusimamia fedha hizi kuona zinapatikana ndani ya halmashauri kwa sababu halmashauri nyingi fedha hii wanasema hizifiki na vijana wengi hawapati fedha hii. Je, kijana huyu unataka kumsaidia kwa njia gani wakati fedha hii haimfikii? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia suala la kiinua mgongo cha Wabunge. Wabunge wengi wameliongelea suala hili la kiinua mgongo cha Wabunge lakini niiombe Serikali yangu, naamini ni sikivu, Serikali ya CCM inavyoambiwa inasikia. Mbunge huyu katika jimbo lake anafanya harusi, maziko, matibabu na kila kitu. Leo hii unasema Mbunge huyu huyu katika kiinua mgongo chake cha mwisho ambacho anakwenda kujipanga kimaisha, umkate kodi, kweli Mbunge huyu unamtaka baadaye afanye kitu gani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yangu kwa nia njema, naamini Serikali yangu ina nia njema, iweze kukaa na kulifikiria suala hili la kuwakata Wabunge kodi. Naamini Serikali yangu ni sikivu na suala hili Wabunge wengi wamelizungumza, watalifanyia kazi.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo inayoweza kumkomboa mwananchi hasa maskini. (Makofi

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia sehemu ya madawa ya kulevya. Tunashuhudia Waziri Mkuu na Wizar aya Vijana jinsi inavyopambana na masuala ya madawa ya kulevya, lakini suala hili kwa kweli bado ni tatizo moja kubwa sana ndani ya Tanzania. Tunaona Mheshimiwa Waziri, askari wanakamata vijana wadogo wadogo kwa issue ya madawa ya kulevya, tunajisahau kuwa vijana wadogo siyo waingizaji wa madawa ya kulevya. Kuna wafanyabiashara wakubwa, kuna viongozi wakubwa, kuna watu maarufu. Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na mapapa hawa na kuachana na ngedere wadogo hawa ambao wao ni watumiaji lakini tunajisahau kama kuna watu ndiyo waingizaji wa madawa ya kulevya; kwa sababu unamkamata kijana mdogo ambae anatumia tu madawa ya kulevya, ukimkamata bado madawa ya kulevya ndani ya nchi yetu yanaendelea kuingia na watumiaji bado wanaendelea kutumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sober house nashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kuna sober houses 22 ambazo tayari zimeanzishwa, lakini sober houses siyo solution ya kusema tunaondoa suala la madawa ya kulevya. Hizi sober house kwanza tukumbuka ni nyumba za watu binafsi, kwa hiyo, business bado inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa vijana waliopo ndani ya sober house wanasema kwamba wakianza kupona baadhi ya sober house wanapewa tena yale madawa ya kulevya ili waendelee kuwepo ndani ya sober house, kwa sababu kijana mmoja aliyopo ndani ya sober house analipia shilingi 400,000, kijana yule akiondoka ile business imeondoka, kwa hiyo, naiomba Serikali ifumbue macho na kuangalia hizi nyumba za sober house ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kama tunataka tuendelee na sober houses ziwekwe ndani ya mwamvuli wa Serikali, hilo ni jambo la kwanza.

Pili, tunataka vijana hawa ambao tayari wameshaathirika na madawa ya kulevya wachukuliwe wapelekwe hospitali, watibiwe, wapatiwe tiba na watakapopona wapewe mtaji badala ya kuwapeleka sober house zile pesa wapewe mtaji kwa ajili ya kuwaanzishia biashara yao, kwa sababu vijana hawa wanakuwa na changamoto za maisha hawana mtaji wa kuanzishia biashara. Zile pesa vijana hawa wapewe kwa ajili ya kuanzisha biashara na wataweza kuachana na madawa ya kulevya na kufanya biashara zao binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ajira. Naomba niongee ukweli kwa sababu nitakapoongea ukweli nitakuwa nimemsaidia Mheshimiwa Rais, tusimdanganye Mheshimiwa Rais tukimdanganya bado tutakuwa hatujamsaidia, ili tumsaidie tumwambie ukweli, vijana wamekosa imani na Serikali yao kwa suala la ajira, suala la ajira limekuwa changamoto tuwatafutie vijana ajira ili waweze kutatua mambo yao wawe na imani na Serikali yao. Tusipoangalia vijana hawa wote watakimbilia kwenye madawa ya kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua Serikali kwamba haiwezi kuajiri vijana wote ambao wanamaliza shule, lakini tuangalie njia gani tutafanya ili kuweza kuwasaidia vijana kuweza kujikwamua na maisha. Kwanza tukae na mabenki, tuzungumze nayo, yapunguze urasimu, yaweze kuwapa vijana mkopo wenye riba nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, benki zina urasimu mkubwa kijana kama mimi nisingekuwa Mbunge leo hii nahitaji mkopo naambiwa niende na hati ya nyumba natoa wapi? Naambiwa niende na hati ya shamba natoa wapi? Ni lazima tukae tufikirie ni njia gani ya kumkwamua kijana aweze kujiendeleza katika maisha yake. Kuna miradi ambayo kuwa Mheshimiwa Rais ameianzisha, lakini unashangaa wanatoka vijana kutoka Kenya, Malawi, sijui kutoka wapi ndiyo anakuja kusimamia ajira hizo, tunaiomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ajira hizi zote zisimamiwe na vijana wa Kitanzania, kama miradi ya umeme iliyoanzishwa Rufiji, standard gauge na ujenzi wa viwanja vya ndege ajira hizi zote tunaomba zipate vijana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu afya ya akina mama; kama mwanamke na kama mzazi nitakuwa sijajitendea haki nisipochangia suala la afya ya akina mama. Tulimuona Naibu Waziri akifungua warsha yake kwa vifungashio vya akina mama na akisema kina mama wachangie shilingi 20,000. Bado kwa mwanamke shilingi 20,000 ambaye ana kipato cha chini ni kubwa sana, kwa nini asiseme vifungaishio hivi viwe bure au aweke shilingi 5000 ambayo anajua mwanamke huyo au mama huyu anaweza kuimiliki kila mwanamke wa kijijini, kila mwanamke maskini anaweza kununua vifunganishio hivi, shilingi 20,000 bado kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu mazingira. Kila siku tunamshuhudia mama yetu Mheshimiwa Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan akienda katika warsha za kuendeleza misitu, tusikate miti hovyo, lakini nikwambie ukweli, miti bado itaendelea kukatwa kwa sababu bei ya gesi bado kubwa sana. Mwananchi wa kawaida huwezi kwenda kumwambia anunue gesi shilingi 50,000 akaacha mkaa shilingi 20,000, miti bado tunayo lakini hatujajua ni jinsi gani ya kuweza kulinda miti yetu. Kwa hiyo, hiyo miti tunayopanda tutashindwa kuilinda kwa sababu sasa hivi hatujui ni jinsi gani ya kuilinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu isaidie akina mama maskini kwa kuweza kupunguza bei ya gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu asilimia 10 inayotokana na vijana, akina mama na asilimia mbili kwa walemavu. Tukiongea ukweli ndani ya Halmashauri yetu hii pesa haipatikani, naiomba Serikali itafute njia ya kuweza kusimamia Halmashauri hizi ili vijana waweze kupata hizi asilimia nne, wanawake wapate asilimia hizi nne, walemavu wapate hizi asilimia mbili jumla itakuwa ni asilimia
10. Halmashauri itakapotenga hii pesa tutakuwa tumepunguza lile tatizo la kusema ajira kwa vijana, watajua jinsi gani kwa sababu ajira zipo nyingi, kijana anaweza kujiajiri kwenye kilimo, uvuvi, lakini kijana huwezi kumwambia leo hii aende akalime kilimo cha locally au aende akavue uvuvi locally lazima atataka kulima kilimo cha kisasa cha kumwagilia maji, kilimo hicho ili uweze kulima uwe na milioni tano isipungue, sasa hizi asilimia 10 zitakazotolewa na Halmashauri zetu vijana hawa wataweza kujisaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la bandari kidogo tu, bandarini pamekuwa na urasimu mkubwa sana, sisi tunaosafiri kupitia baharini pale ndiyo tunaona. Kijana anasafiri na vitenge doti 10 tu anaambiwa sijui TRA achangie, ushuru wa bandari, hebu tufikirie kijana huyu vitenge 10 atapata faida shilingi ngapi, pesa yote ambayo anachajiwa pale bandarini ndiyo pesa yake yote anayopata faida. Kwa hiyo anakuwa anafanya business as usual.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuangalie tena amechangia Bara anaenda Zanzibar anachangia tena, naomba haya mambo tuyaangalie huu urasimu mdogo wa kuondoka na doti 10 hapa za vitenge, halafu kijana yule akienda Zanzibar anakuwa-charged.

T A A R I F A . . .

MHE. MUNIRA MUSTAFA KHATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo tena kwa mikono miwili asilimia mia moja. Hivyo ndivyo ilivyo, tunaomba basi Serikali ikae ifikirie hili suala limekuwa tatizo sana kwa vijana wetu, hawatafika wakati wakaweza kujitegemea wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, ninaunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. MUNIRA M. KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru kwa kupata nafasi kuchangia jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri wake na timu yake yote, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu kwa hotuba nzuri ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kauli yake ya kusema sasa suala la mafuta ndani ya nchi yetu siyo tatizo. Naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipokuwa katika ufunguzi wa Kiwanda cha Singida alisema kuwa viwanda vya kuzalisha mafuta anaondoa VAT kwa asilimia 18. Naomba Serikali iniambie, imetekeleza vipi agizo hili la Mheshimiwa Rais kwa kuondoa VAT katika mafuta ya alizeti?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tunataka tufikie katika uchumi wa viwanda basi la kwanza ni kuvilinda viwanda vyetu vya ndani. Siyo viwanda vya mafuta tu, hata viwanda vyetu vya maziwa, tunaiomba Serikali iweze kuangalia suala hili ya VAT ya asilimia 18. Tutapoondoa asilimia hii 18, kwanza tutaweza kuongeza uzalishaji ndani ya nchi yetu, tutaweza kupunguza kuagiza mafuta ndani ya nchi yetu, tutaweza kuwasaidia wakulima wetu kimaisha ndani ya nchi yetu, hata pia tutaweza kuondoa tatizo la wafugaji kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kuhusu SIDO. Katika taarifa ya CAG, SIDO inaonekana iko katika hali mbaya. SIDO inafanya vibaya ndani ya mikoa yetu na Tanzania kwa ujumla. Mwaka 2017/2018 imepangiwa shilingi bilioni 6 lakini ndani ya pesa hii haijapatikana hata asilimia 1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira nyingi za vijana zinapatikana katika viwanda vidogo vidogo. Kama tungeisaidia vizuri SIDO basi tungeweza kuzalisha ajira nyingi kwa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetembelea SIDO ya Iringa ina wafanyakazi watatu tu ambao wameajiriwa na Serikali. Hivi tutafikiaje uchumi wa viwanda na tunawasaidiaje vijana? Naiomba Serikali iangalie namna ya kuajiri watumishi wa SIDO ndani ya mikoa yetu na wazisaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, SIDO ina wafanyakazi watatu, waliobakia wote wanajitolea mpaka Mnunuzi Mkuu na Mhasibu ndani ya SIDO wanajitolea, hizi kazi zinaendeshwaje? Naiomba Serikali na Mheshimiwa Waziri uko hapo, uisaidie SIDO ili kuweza kufikia katika uchumi wa viwanda. Kama hatuwezi kuzisaidia SIDO zetu, basi hatutaweza kusaidia uchumi wa viwanda. Ndani ya SIDO kuna mashine za miaka 70 kabla mimi sijazaliwa ndizo zinatumika mpaka leo. Naomba hizi pesa ambazo zimetengwa kwa ajili ya SIDO, zifike na zitolewe kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hii FCC imekuwa tatizo sana kwa wafanyabiashara. Wamekaa kwa ajili kupiga penalty tu. Naiomba Serikali wangekaa na hizi taasisi wakawapa wafanyabiashara elimu. Wakienda sehemu za kuchukua bidhaa wajue ni bidhaa gani ambazo zinatakiwa ziingie ndani ya nchi yetu ili wasiwe wanachukua mzigo ambapo kisa tu haukuandikwa Sumsung au haukuandikwa iPhone ukifika ndani ya Tanzania mzigo ule ikawa ni kuharibiana biashara kwa kuchomeana moto. Tungekaa tukafikiria, kuna wafanyabiashara mpaka wanaumwa, wengine wanakufa kwa sababu ya hii FCC. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri akae basi aangalie Watendaji wake aweze kuwasaidia wafanyabiashara wengi. Juzi kontena nzima ya chupi imechomwa moto na FCC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna viwanda vimebinafsishwa ambavyo vilikuwa haviwezi kufanya kazi.

Naiomba basi Serikali viwanda vile virudi katika mikono ya Serikali. Viko ambavyo havijabinafsishwa lakini vinamilikiwa na sekta binafsi na zipo share za Serikali. Naiomba basi Serikali ikaangalie viwanda hivi ili viweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi niliuliza swali hapa kuhusu Kiwanda cha Nguo cha Urafiki lakini sikupata majibu ya kutosha na ndani ya kitabu cha Mheshimiwa Waziri sikuona maelezo yoyote kuhusu kiwanda hiki. Naomba basi wakati anahitimisha aniambie suala hili la Kiwanda cha Urafiki limefikia wapi kuhusu zile shares ambazo tunazo na wenzetu wa China? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kiwanda cha Nyama Dar es Salaam, naomba Mheshimiwa Waziri akiwa anahitimisha pia aje aniambie. Pia kuna Kiwanda cha ZZK Mbeya, kilikuwa kinatengeneza vifaa vya kilimo. Naomba Mheshimiwa Waziri akija aniambie, kwa sababu mpaka sasa hivi wakulima wetu kutumia majembe ya mkono wakati sisi wenyewe tulikuwa tuna kiwanda kikubwa tu na hakifanyi kazi, itakuwa ni aibu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aniambie kuhusu viwanda hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili la vinywaji vikali ambapo Serikali inapoteza kodi nyingi. Vinywaji hivi vikali vinakosa kodi kwa kubandika sticker bandia na hili suala kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameliongea na ushahidi upo. Naomba basi Serikali iangalie inapoteza mapato kiasi gani katika suala hili la kubandika hizi sticker bandia katika vinywaji vikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vinywaji vikali Serikali ingekuwa ina-charge ile spirit wakati inaingia hapa nchini badala ya spirit ikiwa imeshatumika ndani ya vinywaji vikali ndiyo inakuja kuchajiwa. Hizi spirit zinapoingia tu nchini zichajiwe. Kwa sababu hizi spirit zinachajiwa kwa kiwango kidogo tu zinazokwenda kwenye hospitalini na sehemu nyingine lakini kiwango kikubwa kinatumika katika vinywaji vikali. Kwa hiyo, Serikali ingekaa ikaangalia vizuri kwa upande wa spirit inapoingia nchini. Tusi-charge ndani ya vinywaji, bali tu-charge inapoingia tu ndani ya nchi yetu.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi kwa kuweza kunipatia nafasi ya kuweza kuchangia bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niweze kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kaka yangu Mwigulu Nchemba, lakini nimpongeze sana Naibu Waziri wa Fedha, kaka yangu Mheshimiwa Engineer Hamad Masauni, lakini niweze kumpongeza sana Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na timu yake yote kwa pamoja kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa kutuletea bajeti ambayo inaenda kumgusa mwananchi mwenye kipato cha chini moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Tanzania, Mheshimiwa Mama yangu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa aliyoifanya ndani ya miezi mitatu, hakika natuheshimisha wanawake wote wa kitanzania, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kuangalia suala la Liganga na Mchuchuma kwa sababu ndani ya Bunge hili limeongelewa kwa muda mrefu toka sijawa Mbunge mpaka nimekuwa Mbunge, hiki ni kipindi changu cha pili, awamu zote mbili kwa sasa yeye ndio at least ameamua kuliingilia suala hili. Na suala hili litakapofanikiwa kufufua Liganga na Mchuchuma vijana wataweza kupata ajira kwa wingi, lakini tutaweza kununua pembejeo kwa wakulima wetu, lakini pia tutaweza kutengeneza barabara zetu kwa pesa zetu za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumpongeza pia Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kufuta tozo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu asilimia sita, lakini kama mimi ni Mbunge wa vijana kama sijawasemea vijana wenzangu nitakuwa sijawatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kiukweli juzi alituonesha upendo wa dhati Jijini Mwanza siku ya tarehe 16 na alituahidi mambo mazuri ambayo kwa sisi kama vijana atatupatia. Niseme ahsante sana, lakini naomba niyanukuu mambo machache kwa ufupi ambayo ametuahidi kama vijana; kuwajengea mazingira mazuri ya kufanyia biashara, kuwapa ujuzi, mazingira bora ya kufanyia kazi ya uzalishaji, lakini kubwa zaidi kusubiria mkeka wa ma-DC, ma-DAS na Wakurugenzi ambao wengi wao watakuwa wanatokana na vijana. Nimuahidi Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuwa sisi vijana tuko nyuma yake na hatutamuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa kumaliza tatizo la kuunganishwa kiuchumi kati ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar kwa kutunga sheria ya kuondoa kodi kulipia mara mbili. Nishukuru sana Serikali yangu, lakini bado kumekuwa na changamoto kuhusu wafanyabiashara wa Kizanzibari wamekuwa wakilalamika kwa muda mrefu sasa kuhusu mfumo wa kodi uliokuwepo sasa hivi. Niiombe Wizara ya Fedha iweze kuangalia upya kuhusu mfumo wetu wa kodi kwa wafanyabiashara wetu wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala Wabunge wengi hasa kutoka Zanzibar, wameliongelea na mimi nikiwa mmojawapo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha hebu tukae tuangalie Zanzibar na Tanzania Bara ni nchi moja, lakini sijui kwa nini kumekuwa na ukiritimba katikati ambao haueleweki kati ya wafanyabiashara wetu kutoka Zanzibar kuwa-charged tena mara mbili kati ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania Zanzibar tayari wameanza kufanya marekebisho ya Sheria ya VAT kwa kuondoa tozo mpaka kufikia asilimia sifuri, lakini kwa bidhaa za viwandani peke yake. Hii haijaidia kwa mfanyabiashara ambaye hana bidhaa za viwandani na niishauri Serikali hata ikiwezekana kuiruhusu sukari yetu ya Zanzibar kuuzwa Tanzania Bara kama itawapendeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Mheshimiwa Waziri wa Fedha amependekeza kodi mpya inayotokana na simu pamoja na mafuta ili kuweza kupata fedha kwa miradi ya kimaendeleo. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri wa Fedha wa Tanzania Bara, je, amewasiliana na Waziri wa Fedha Tanzania Zanzibar kuhusu mgawanyo wa miamala na matumizi? Kwa sababu kwa upande wa Zanzibar bado sijaona kitu chochote kuhusu kodi hii inayotokana na mafuta na simu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa mwaka tutakusanya zaidi ya shilingi trilioni mbili kwa tozo zinazotokana na sim una mafuta. Hizi fedha ni nyingi sana, ili Watanzania wawe na imani ya kuchangia fedha hii ni lazima Wizara iweke wazi jinsi ya kutumia fedha hii, lakini nataka niishauri Serikali kwanza kuwa na uwazi jinsi miradi itakayotumika kwa fedha za tozo hii ya mafuta na simu, lakini pia kuwe na ukaguzi wa CAG tena wa mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Mheshimiwa Waziri, hivi karibuni tumemuona Mheshimiwa Waziri Mkuu akitumbua wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, aliwasimamisha kazi kutokana na matumizi mabaya ya fedha ambayo yalikuwa yanatumika bila ya mpangilio maalum. Ndio maana nimesema hizi fedha ambazo zitakusanywa zikaguliwe na CAG tena ikiwezekana mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu upungufu wa wafanyakazi wa TRA. Nimemsikia Mheshimkiwa Waziri kuwa tutaweza kuajiri wafanyakazi 40, lakini niseme jamani wafanyakazi 40 ni wachache sana. Mimi binafsi nilikuwa katika Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira nimeona jinsi watu wa TRA wanavyolalamika kuhusu wafanyakazi wao, tunapoteza sana mapato ya Serikali kwa sababu watumishi ni kidogo. Niiombe Serikali iweze kutoa kibali cha kuajiri wafanyakazi wengine wapya tena wenye weledi na uelewa wa jinsi ya kuweza kukusanya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2020/2021 tumekusanya shilingi trilioni 14.52 sawa na asilimia 82 tu; bado malengo ya Serikali hatujafikia. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweze kuajiri watumishi wa TRA ili kuweza kupata fedha zaidi kwa sababu sasa hivi wamekuwa hata wananchi zamani ilikuwa kuna elimu mwananchi aweze kudai risiti ya kielektroniki, lakini sasa hivi mwananchi mfanyabiashara hawatoi risiti za kielektroniki na tunaweza kupoteza kodi kubwa ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie, nimeona matairi ya pikipiki tayari yameongezewa charge ya VAT, lakini sasa hapa Tanzania tunakiwanda chetu cha General Tyre ambacho tulikuwa tunazalisha matairi. Niiombe Serikali kama kweli tuko tayari kuwasaidia vijana na ajira tungeangalia suala la kufufua kiwanda hiki cha General Tyre kilichopo Arusha. Toka mimi sio Mbunge kiwanda hiki cha General Tyre kinapigiwa makelele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekunde 30; naomba nipongeze sana Wizara hii na niseme inaenda kufufua uchumi wa mwananchi, vyuma vinakazuka chini ya Rais mwanamke Mama Samia Suluhu Hassan. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. MUNIRA MUSTAFA KHATIBU: Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mungu kwa kunijalia afya njema. Aidha, nampogeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake katika kushughulikia tatizo la maji nchini.

Mheshimiwa Spika, juhudi za Mheshimiwa Rais zinaonesha wazi dhamira yake ya kutua ndoo kichwani wanawake ambao ni waathirika wakubwa wa tatizo la maji. Hatua hizi za Mheshimiwa Rais zinaonekana kupitia namna alivyotoa fedha za miradi ya maendeleo ya maji.

Mheshimiwa Spika, miradi ya maendeleo; katika mwaka 2022/2023 Wizara ya Maji - Fungu 49 ilitengewa shilingi 657,899,338,000; kiasi hicho kinajumuisha shilingi 407,064,860,000 fedha za ndani na shilingi 250,834,478,000 fedha za nje.

Mheshimiwa Spika, hadi mwezi Aprili, 2023 Wizara imepokea jumla ya shilingi 623,753,326,424.64 sawa na asilimia 94.81 ya bajeti iliyoidhinishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa mwaka 2022/2023; kati ya fedha zilizopokelewa shilingi 374,794,312,195.31 sawa na asilimia 92.07 ni fedha za ndani na fedha za nje ni shilingi 248,959,014,229.33 sawa na asilimia 99.25.

Mheshimiwa Spika, kwa namna fedha zilivyotolewa na Mheshimiwa Rais ni wazi kuwa amelenga kuondoa changamoto ya maji nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kutoa fedha za kutosha katika Wizara hii, bado kuna changamoto kadhaa ambazo zinaathiri malengo yaliyokusudiwa. Changamoto hizo ni kama ifuatavyo; upatikanaji wa maji katika Jiji la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi za Serikali, tatizo la maji Dodoma limeendelea kuumiza wananchi kutokana na uhitaji wa maji. Mahitaji hayo yanatokana na ongezeko la wananchi waliohamia Dodoma na kuanzisha makazi. Hali ilivyo sasa maji yanatolewa kwa mgao wa mara tatu kwa wiki hali ambayo inarudisha nyuma maendeleo hasa kwa wale wananchi wanaojishughulisha na biashara ya maji na sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi za Serikali za kuondoa changamoto hizo kwa kuanza mpango wa kuleta maji kutoka Bwawa la Mtera na kujenga bwawa jipya la Farkwa, hatua hiyo haijaonesha dhamira ya muda mfupi ya kuondoa tatizo hilo. Nashauri Wizara kuharakisha mchakato wa kukamilisha hatua za ujenzi wa miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu changamoto ya wakandarasi kuchelewa kulipwa; kumekuwepo na changamoto ya wakandarasi kutekeleza miradi bila kulipwa fedha zao kwa wakati hali ambayo imesabisha miradi kuchelewa kukamilika na nyingine kukwama na kuongeza gharama za utekelezaji wa miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kulipa madeni ya wakandarasi kwa wakati ili miradi ya maji iweze kukamilika kwa wakati.

Kuhusu changamoto ya wakandarasi kupewa mradi zaidi ya mmoja; taarifa zinaonesha kuwa moja ya changamoto kubwa ya kutokukamilika kwa miradi ya maji nchini ni pamoja na mkandarasi mmoja kupewa mradi zaidi ya mmoja. Hali hiyo imesababisha wakandarasi wengi kushindwa kukamilisha miradi hiyo kwa wakati kwa kuwa wamekuwa wakihamisha mashine na nguvu kazi kutoka mradi mmoja kwenda mradi mwingine.

Mheshimiwa Spika, tatizo hili linasababisha hasara kubwa kwa Serikali kutokana na miradi kuchelewa kukamilika na kusababisha ongezeko la gharama za vifaa. Hivyo ni rai yangu kuwa Wizara itaangalia suala hili kwa kina katika mipango ijayo ya miradi ya maji nchini.

Mheshimiwa Spika, mwisho nampongeza Waziri wa Maji Mheshimiwa Jumaa Aweso na Naibu wake Mheshimiwa Maryprisca Mahundi kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika,naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum. Kwanza kabisa, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wizara kwa ujumla. Tunawapongeza sana, wanafanya kazi kubwa kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya, kuifungua nchi kiuchumi. Pia nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuwaamini vijana na kuweza kuwapatia ajira zaidi ya 21,000 kwa kada japo ni tofauti, ikiwepo Ualimu na Udaktari. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais na niseme, sisi vijana tuko pamoja naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nielekeze mchango wangu kuhusu watoto waliofanya makosa, waliopo gerezani. Kiukweli watoto ambao wanahukumiwa na kupatiwa adhabu walioko gerezani wengi wao wanafanya wakiwa na umri mdogo. Wanafanya makosa wakiwa na umri wa kuanzia miaka nane hadi 18. Wengi wao wanakuwa chini ya umri wa miaka kumi na nane.

Mheshimiwa Spika, adhabu zinazotoka kwa watoto hawa ni kali. Adhabu zao zinaanza kwa kufungwa jela kwa miaka thelathini, wengine wanahukumiwa kwa kifungo cha maisha, wengine wanahukumiwa kunyongwa. Tukumbuke mtoto huyu anafanya kosa akiwa na umri wa utoto. Mara nyingi wanafanya makosa ya mauaji, lakini kifungo wanachokitumikia ni cha muda mrefu. Je, Serikali inahakikisha vipi wanapata stahiki zao watoto hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, watoto hawa ambao wako kwenye magereza wanakosa zile haki za Watoto. Kwanza kusoma, hawasomi vizuri; kulala, mazingira yao kama watoto bado wanastahiki kulala sehemu nzuri, lakini wanakosa huduma hii ya kulala sehemu nzuri. Japo Serikali imeonesha ina nia na dhamira ya kuendelea kujenga magereza ya watoto, lakini toka bajeti iliyopita Wizara imeendelea kusema itajenga magereza ya watoto, lakini bado hawajaweka miundombinu na miundo rafiki kwa watoto hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukumbuke adhabu hii kwa watoto wetu ni ngumu sana. Naiomba sana Wizara hii kupitia Bunge lako tukufu, ije na muswada wa kurekebisha sheria hizi ili kuwe na adhabu ya watoto. Kwa mfano, mtoto ameua akiwa na umri wa miaka nane, jifikirieni ninyi Waheshimiwa Wabunge nyote hapa, mkiwa na umri wa miaka nane, mlikuwa mnakumbuka nini? Sidhani kama kuna Mbunge alikuwa anajielewa akiwa ameshafanya makosa haya akiwa na umri wa miaka nane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, adhabu hizi ni kali, tuangalie, kwa mfano kuna msanii mmoja anaitwa Lulu, alimuua Kanumba, lakini amepatiwa adhabu ambazo ni za kiutoto na ametoka, lakini kuna watoto wengine mpaka leo wako magerezani. Wamefanya kosa lile lile la kuua. Tuangalie, kama leo Kanumba angekuwa hai, leo hii angekuwa naye anahukumiwa kwa kosa la kubaka miaka 30 jela.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Wizara hii iendelee kuangalia watoto ambao wako magereza, adhabu hizi siyo rafiki kwa watoto. Tuangalieni upya, tulete adhabu za watoto ambazo hata wakitoka jela wanaweza kufanya kazi zao za kiuchumi. Leo unamhukumu mtoto akiwa na miaka mitano, umemhukumu akae jela miaka 30, ametoka jela akiwa na miaka 35. Je, unafikiria umemjengea mazingira gani katika jamii yake? Kusoma hajui, biashara hawezi kufanya, atafanya kitu gani? Tunamfanya aingie tena kwenye makundi ya wizi, kwa sababu kule gerezani hakupatiwa elimu na kuweza kujisaidia yeye mwenyewe ili kipindi akitoka jela aweze kujisaidia. Naiomba sana Wizara iweze kuangalia. watoto wanafanya makosa, ni kweli hatukatai, lakini wanafanya makosa wakiwa na umri wa watoto pasipo kujielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la udhibiti wa hizi taasisi zisizokuwa za kiserikali. Hivi karibuni tumeshuhudia shughuli ambazo zinafanywa na taasisi zisizokuwa za kiserikali (NGOs). Ni kweli tunazitaka NGOs kwenye nchi yetu ya Tanzania, lakini zipo nyingine hazina lengo zuri kwa jamii zetu. Taasisi hizi zinapotosha watoto wetu, tukae tuziangalie upya. Tuna shida gani kuzifutia leseni taasisi ambazo tunahisi zinahamasisha ushoga? Tukae, tufikirie. Naiomba Wizara iangalie kwa ukaribu na ifuatilie kwa ukaribu mashirika haya ambayo tunahisi yako kinyume na maadili ya kitanzania yafungiwe kwa haraka, kwa sababu bado yapo yanaendelea na yanaendelea ku-support suala la ushoga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunalalamikia mashoga, lakini hatuangalii chimbuko lake ushoga unatoka wapi? Kama tungekuwa tunaangalia ushoga unatokea wapi, tunadhibiti nini, basi tusingefikia huku kwa sababu hakuna shoga ambaye anaweza kuwa mtu mzima akaibuka kuwa shoga. Ushoga unaanzia utoto. Huwezi kuwa shoga mtu una miaka 30 au 35. Ushoga lazima utaanza ukiwa mtoto na kijana, ili ukifika miaka
30 tayari umekomaa kuwa shoga. Naiomba sana Wizara iendelee kuangalia taasisi hizi ambazo haziitakii nchi yetu mema, na kuzifungia taasisi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana katika mitaala yetu ya elimu, tunajua sasa hivi kuna marekebisho ya mitaala ya elimu, lakini tuangalie shule za msingi, watoto wetu waanze kufundishwa somo la ukatili wa kijinsia ili waweze kujitambua na kujikinga na ukatili. Kama tutawafundisha watoto wetu mapema, likiingizwa kama somo, watoto wetu wataelewa unapofanyiwa hivi ni udhalilishaji; na unapofanyiwa mambo haya uripoti wapi. Kama hatujafanya hivyo, hatuwezi kuwalinda watoto wetu. Mtoto hajijui kama hiki ninachofanyiwa ni udhalilishaji, wapi niripoti? Leo tunawaimbisha watoto sawa, ukifanya hapa don’t touch me, ukiguswa hapa don’t touch me, lakini bado hatujawapa uelewa zaidi. Tuendelee kwenye mashule kuweka kama subject ili watoto wetu waweze kujitambua.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Munira kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Festo Sanga.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, anachokiongea Mheshimiwa Mbunge ni sahihi kabisa kwa sababu hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 30 wanasema wamefungua madawati 1,500 na kitu kwenye shule za msingi, na tunajua walimu wengi wana vipindi. Ni wakati sahihi sasa wa Serikali kuajiri Maafisa Ustawi Wajamii wengi kwa ajili ya kila shule kwa ajili ya kusaidia watoto wetu, kwa sababu walimu ni wachache, hawawezi kufanya hiyo kazi. Kwa hiyo, tukiajiri Maafisa Ustawi wa Jamii, wanaweza kusaidia hili jambo, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Munira na muda wako umekwisha. Inapokea taarifa hiyo?

MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo lakini tuzingatie zaidi kuanzisha masomo haya kwenye elimu zetu za awali.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kwa kuweza kunipatia nafasi ya kuweza kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Nimpongeze sana amepambana sana na panya road na sasa hivi Tanzania yetu imetulia, majangili wamepungua. Kwa hiyo nimpongeze sana kaka yangu Masauni, endelea kufanya kazi sisi tunakuamini na Taifa linakuamini pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti,napenda kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wizara yote kwa ujumla, hakika mnafanya kazi nzuri sana, nawapa pongezi sana. Lakini niwapongeze sana sana Wizara kwa kuanza ujenzi wa kituo changu cha Wilaya Mkoani. kituo hiki kilikuwa kimezungushwa mabati tangu mwaka jana lakini huu mwezi wa tano sijui kwa ajili ya bajeti ya leo tayari kimeanza msingi na tayari kimeanza kufanyiwa kazi. Niombe Serikali, itakapo pita bajeti hii kile kituo basi kiendelee pia na ujenzi wake usije ukasita. Iendelee na kile kituo pale kimalize kwa sababu kituo hiki ni kituo muhimu, ndicho kituo ambacho kimezungukwa na Bandari ya Mkoani pale, kwa hiyo ni kituo muhimu sana. Ujenzi wake naomba uendelee na uharakishwe zaidi kwa sababu ni kituo muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na kituo hiki, niombe nyumba za Wilaya Mkoani, Waheshimiwa Wabunge karibu wote wamezungumzia hapa suala la nyumba. Suala la nyumba limekuwa ni tatizo kwa Tanzania nzima. Niombe basi Wizara iweze kuangalia upya suala la nyumba ya makazi ya askari hawa. Hasa ukiangalia mazingira ya Pemba. Mazingira ya Pemba si rafiki askari kukaa uraiani. Ukiangalia mwaka sasa hivi tulionao tunapitisha bajeti ya 2023/2024. Mwaka kesho tu kuna uchaguzi. Si mazingira rafiki kwa askari wetu kukaa katika nyumba za uraiani. Niombe sana Serikali iweze kuangalia upya suala la nyumba za mapolisi, naamini Serikali yangu ni Sikivu.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mheshimiwa Saashisha taarifa ya tatu leo inatosha hiyo. Mheshimiwa Mnura endelea na mchango wako.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba suala la nyumba hili Serikali yangu Sikivu itasikia na itafanyia kazi. Mheshimiwa Waziri tunakuamini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la dawati la jinsia. Nipongeze sana. Serikali kwa kuamua kwa makusudi kuunda hili dawati la kijinsia la watoto ndani ya Jeshi la Polisi. Kwa kweli mmetusaidia wazazi na hili dawati linafanya kazi nzuri sana. Lakini niombe Serikali, dawati hili liwe na kamisheni, liweze kujitegemea lenyewe na liwe na bajeti ya kutosha. Hatuwezi dawati hili kulichanganya ndani ya askari jamii kwa sababu dawati hili linafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri akae aangalie dawati hili lina wasaidia watoto. Mimi binafsi nimeshaenda kulitembelea dawati hili, linatoa elimu, linawasaidia akina mama, linafanya kazi zake vizuri. Dawati hili linatakiwa liweze kujitegemea. Kama ilivyo kwa askari jamii ndivyo dawati hili linatakiwa lijitegemee lenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tunataka kumaliza suala la udhalilishaji kwa watoto basi ni lazima kuweza kuwapa kamisheni iweze kujitegemea wenyewe lakini pia dawati hili lipatiwe fedha ya kutosha ndipo litaweza kufanya vizuri. Kwa sababu sasa hivi tunapokwenda kuna mambo mengi ya udhalilishaji wa kijinsia kama tutalisaidia dawati hili, yale masuala mengi ya ukatili wa watoto naamini yatapungua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Munira ahsante sana muda…

MHE. MUNIRA MUSTAPHA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba niunge mkono hoja.