Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Maria Ndilla Kangoye (13 total)

MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Tanzania kuna mashirika makubwa yasiyo ya Kiserikali ambayo yanaisaidia sana Serikali katika kuwahudumia wananchi hasa wanawake misaada ya Kisheria. Mfano wa Mashirika haya ni TGNP, LHRC, WILDAF, TAWLA, lakini yanafanya kazi kwa kutegemea ufadhili wa wahisani kutoka nchi za nje:-
(a) Je, ni lini Serikali itatenga asilimia kidogo ya pato lake kuyapatia ruzuku mashirika haya kama Serikali inavyotoa kwa vyama vya siasa?
(b) Je, ni lini Serikali itayahamasisha mashirika na makampuni ya ndani nayo kuona umuhimu wa kuingia nayo mikataba ya ushirikiano ili kutoa huduma kwa kiwango kikubwa zaidi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua haja ya kufanya kazi kwa ubia na mashirika yasiyo ya Kiserikali na pia kuyapatia ruzuku kwa ajili ya kuwahudumia wananchi. Kwa kuzingatia azma hiyo, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia mikutano mbalimbali ya wadau imekuwa ikihamasisha Taasisi za Serikali kufanya kazi kwa ubia na mashirika haya, kama inavyoainishwa katika Sera ya Taifa ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali. Kutokana na jitihada hizo, baadhi ya Taasisi za Serikali ikiwemo Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Wizara, Idara na Wakala za Serikali zimeanza kutoa ruzuku kwa mashirika haya.
Kwa mfano, katika miaka ya hivi karibuni Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI, Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Kimataifa na Halmashauri mbalimbali zimekuwa zikitoa ruzuku kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yanayojishughulisha na masuala ya VVU na UKIMWI, Maadili na Mazingira. Mfano mwingine ni Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ambayo katika mwaka 2015 ililiwezesha Shirika la Mbozi Society for HIV/AIDS Campaign and Social Economic Development kwenda vijijini kutoa elimu ya VVU na UKIMWI.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Serikali kuhamasisha mashirika na makampuni ya ndani kuingia mikataba ya ushirikiano na Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, kupitia mikutano baina ya Bodi ya Uratibu wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali na wadau mbalimbali iliyofanyika katika mikoa 22 ya Tanzania Bara, imekuwa ikihamasisha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuanzisha ushirikiano na ubia na Serikali pamoja na sekta binafsi, ikiwemo makampuni.
Kutokana na jitihada hizi, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yameanza kufanya kazi kwa ubia na makampuni mbalimbali hapa nchini. Mfano mzuri ni Shirika lisilo la Kiserikali la Mbalawala Women Organisation (MWO) linalofanya kazi kwa ubia na Kampuni ya Tancoal Energy Limited katika kukuza ajira ya wanawake kwenye vya Ntunduwaro na Ruanda, Wilayani Mbinga, Mkoani Ruvuma.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Sekta ya Utalii ni Sekta inayotegemewa kuliingiza Taifa mapato kwa sababu ya vivutio vingi tulivyojaliwa Tanzania:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutekeleza ahadi iliyopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2016 - 2020 katika kuongeza bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii?
(b) Je, ni nini mkakati wa Serikali kukiimarisha Chuo cha Utalii ili kutoa mafunzo ya Hoteli na Utalii katika ngazi ya Stashahada ili kuongeza ubora wa Watumishi wa huduma za ukarimu na utalii?
(c) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuweka mazingira bora ya kuwezesha vijana kuanzisha makampuni ya kutembeza watalii katika maeneo mbalimbali ya utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2016 -2020, katika Ibara ya 29(c) inaainisha azma ya Chama cha Mapinduzi kusimamia Serikali katika utekelezaji wa mikakati ya kukuza utalii nchini kwa kuhakikisha kwamba bajeti ya Sekta ya Utalii inaongezeka ili kuutangaza utalii ndani na nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza mkakati huo, Wizara yangu kupitia Bodi ya Utalii na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania imetenga jumla ya sh. 2,730,188,676/= kwa ajili ya shughuli za utangazaji kwa mwaka wa fedha 2016/2017, hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 14.7 ikilinganishwa na mwaka 2015/2016. Serikali itaendelea kuboresha utekelezaji wa ahadi hii kwa kushirikisha pia wadau mbalimbali wa maendeleo na vyanzo vingine kama inavyoainishwa na mpango wa maendeleo wa miaka mitano 2016/2017 – 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali katika kukiimarisha Chuo cha Utalii katika Kampasi zake zote tatu za Bustani, iliyoko Dar es Salaam; ya Temeke iliyoko Dar es Salaam pia na ya Arusha. Ni pamoja na kuongeza idadi na umahiri wa wakufunzi, kuboresha upatikanaji wa vifaa mbalimbali vya kufundishia na kuboresha miundombinu ya chuo katika kampasi zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mipango ya hivi karibuni Chuo cha Utalii kitaboresha utoaji wa mafunzo katika Tasnia ya Ukarimu (Hospitality) na Utalii (Tourism) katika ngazi ya Shahada.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Chuo cha Utalii kwa kushirikiana na Chuo cha Vancouver Island University cha Canada kupitia Mradi wa ISTEP chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kitaanzisha mafunzo ya uongozi katika ngazi ya Shahada kuanzia mwezi Septemba, 2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uimarishaji wa miundombinu, Wizara yangu imetenga jumla ya shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2016/2017 ili kukamilisha ujenzi wa jengo la Utalii (Utalii House) Phase II katika Kampasi ya Bustani ya Chuo cha Utalii, Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mazingira bora ya kuwezesha vijana kuanzisha makampuni ya kutembeza watalii katika maeneo mbalimbali ya utalii; Serikali itaendelea kwa msisitizo zaidi kushirikisha sekta binafsi ili kuwashauri vijana wajiunge katika vikundi na kuwapa elimu ili waanzishe na kushiriki kwa tija zaidi katika biashara hii kwa maslahi yao na kwa maslahi ya Taifa. Serikali pia itapitia masharti yote yaliyopo kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu ili kuona kama kutakuwa na uhitaji wa kuyafanya masharti hayo kuwa rafiki zaidi kwa vijana wenye nia thabiti ya kushiriki katika ujenzi wa uchumi wa Taifa kupitia shughuli za uongozaji watalii.
MHE. HAWA M. CHAKOMA (K.n.y. MHE. MARIA N. KANGOYE) aliuliza:-
Viongozi wa Dini wanaheshimika sana, wanahimiza utulivu na amani na kuliombea Taifa letu. Hata wakati wa kumwapisha Rais, Viongozi hawa hupewa nafasi ya kumwombea Rais na kuiombea nchi:-
(a) Je, ni lini Serikali itatoa umuhimu kwa Viongozi Wakuu wa kidini kupewa hadhi ya kupitia sehemu ya Viongozi wenye heshima (VIPs) katika viwanja vya ndege na sehemu ambazo kuna huduma kama hizo?
(b) Je, ni vigezo gani au utaratibu gani unaotumika kuwapa Hati za Kidiplomasia watu mbalimbali, lakini viongozi wetu wa kidini hawana hadhi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya Kumbi za Watu Mashuhuri, (VIPs Lounge) hasa katika viwanja vya ndege nchini, huratibiwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Utaratibu ni kuwa, Kiongozi wa Dini au mtu yeyote anayestahili kutumia sehemu hizo, hujaza fomu za kuomba kutumia na Wizara yangu imekuwa ikitoa vibali vya matumizi ya sehemu hizo pindi itokeapo maombi hayo ikiwa ni pamoja na Viongozi Wakuu wa Dini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa hati na nyaraka za kusafiria za aina zote hufanywa kwa kufuata Sheria Na. 20 ya mwaka 2002 ya Hati na Nyaraka za Kusafiria ijulikayo kama Passports and Travel Documents Act, No. 20 of 2002.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa mujibu wa Kifungu cha 5 (1) cha Sheria hiyo, Mkurugenzi wa Uhamiaji ndio mwenye mamlaka ya kutoa hati zote za kusafiria. Hata hivyo, Kifungu cha 5 (2) (a) kinamruhusu Mkurugenzi wa Idara ya Uhamiaji kumpa uwezo, yaani ana- delegate kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuelekeza utoaji wa pass za kusafiria za kidiplomasia, (power to authorize grant of diplomatic passport).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 10(3) cha Sheria tajwa kinaelekeza kuwa, wanaostahili kupewa Hati za Kidiplomasi wanapatikana katika jedwali Na. 3 katika Kifungu cha “ddd”, ambapo Mkurugenzi wa Uhamiaji amepewa mamlaka ya kutoa Pass ya Kidiplomasia kwa Viongozi Wakuu wa Taasisi za Kidini hapa nchini kwa kadri anavyoona inafaa. Hivyo, viongozi Wakuu wa Dini wamekuwa wakipewa Pass za kusafiria za Kidiplomasia kulingana na kipengele hicho hapo juu na kwa namna ambavyo mamlaka inayosimamia inavyoelekeza katika sheria husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kulieleza Bunge lako Tukufu kuwa, Pass ya Kidiplomasia ni nyaraka maalum inayomwezesha mhusika kufanya kazi zake hasa za kidipolmasia.
Aidha, Wizara yangu kwa kushirikiana na Mamlaka nyingine husika zinapitia upya Sheria hii ya Pass na Nyaraka za Kusafiria kwa lengo la kuifanyia marekebisho kwa kuangalia pia uzoefu wa nchi nyingine juu ya nyaraka hii muhimu. Pindi zoezi hili litakapokamilika, mapendekezo ya marekebisho hayo yatawasilishwa katika Bunge lako Tukufu kwa ajili ya kuridhiwa.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Kumekuwepo uhaba wa watumishi katika Halmashauri nyingi nchini ambao unaleta athari katika utekelezaji wa shughuli za Halmashauri kwa kutotoa huduma katika kiwango kinachohitajika.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuajiri wataalam hasa vijana waliomaliza vyuo ambao wanazurura mitaani kwa ukosefu wa ajira?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jitihada za kukabiliana na upungufu wa watumishi wa umma Serikali imekuwa ikitenga bajeti ya ikama na mishahara na kutoa vibali vya ajira mpya kwa taasisi zote za umma ikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa, kama ilivyo kwa sekta zote za ajira katika utumishi wa umma kwa kutegemea kiwango cha kukua kwa uchumi. Kwa kuzingatia sera za kibajeti, Serikali imetenga pia nafasi za ajira mpya katika mwaka wa fedha 2016/2017 ambapo zitajazwa kwa awamu, ambapo watumshi wa umma wapatao 5,074 hadi sasa wameshaajiriwa, ikiwemo watumishi wa hopsitali mpya ya Mloganzira. Aidha, tayari Serikali imetoa kibali cha kuajiri walimu wa masomo ya hisabati, sayansi, mafundi sanifu wa maabara za shule za Serikali wapatao 4,348.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kutoa rai kwa mamlaka za ajira kutumia vizuri rasilimali watu walizonazo kwa kuwapanga watumishi wa umma kwa kuzingatia uwiano sahihi ili kuweza kukabiliana na changamoto za upungufu wa watumishi wa umma.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Serikali kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 - 2020 iliahidi kuimarisha huduma za ugani na mafunzo kwa kuongeza udahili wa Maafisa Ugani wa Uvuvi kutoka 1200 hadi 2500 kwa mwaka ili kuwepo Maafisa Ugani kwa ngazi ya kata na kuimarisha huduma za uvuvi na ufugaji samaki.
(a) Je, ni lini mkakati wa utekelezaji wa suala hili ambao utatoa ajira nyingi kwa vijana utaanza?
(b) Je, kuna mkakati gani wa kuzishirikisha Halmashauri nyingi katika kuhamasisha uchimbaji wa mabwawa na ufugaji wa samaki hasa katika maeneo yenye ukame ili kuongeza lishe bora na pia ajira kwa vijana?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa kuongeza za udahili ili kuongeza Maafisa Ugani wa Uvuvi ulianza kwa Wizara kuimarisha Wakala wa Elimu ya Mafunzo na Uvuvi (FETA) katika Kampasi zake za Mbegani (Bagamoyo), Nyegezi (Mwanza), Kibirizi (Kigoma), Mwanza South (Mwanza). Vilevile ili kuongeza udahili wa wanafunzi Serikali itakamilisha ujenzi wa kampasi za Mkindani (Mtwara), Gabimori (Rorya) ifikapo mwaka 2019 ambapo kwa ujumla vyuo vyote vitadahili wanafunzi 2,200 kwa mwaka ukilinganisha na wanafunzi 1,200 wanaodahiliwa kwa mwaka hivi sasa. Vyuo hivyo vinazalisha wataalam wa uvuvi katika ngazi ya Astashahada na Stashahada ambapo hupata ajira Serikalini, sekta binafsi na wengine hujiajiri wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa imechimba visima virefu 101 kwa ajili ya kujaza maji kwenye mabwawa ya kufugia samaki na malambo 1,381 kwa ajili ya kunyweshea mifugo ambayo pia hupandikizwa samaki. Mabwawa hayo yamechimbwa katika Halmashauri mbalimbali nchini hususan maeneo kame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati huu wa kuwezesha ufugaji wa samaki unafanywa kupitia mkakati wa kuendeleza ufugaji katika sekta ya uvuvi 2010. Mkakati wa Taifa wa kuendeleza ufugaji wa samaki na viumbe wengine kwenye maji wa 2009 na Mpango Mkuu wa Sekta ya Uvuvi wa mwaka 2002 (The Fisheries Master Plan, 2002).
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mkakati wa ufugaji wa samaki umepewa kipaumbele katika mpango wa kuendeleza Sekta ya Kilimo (ASDP-2) utakaoanza hivi karibuni. Mikakati yote inatekelezwa chini ya Mpango wa D by D, yaani Ugatuaji wa Madaraka ambapo utekelezaji wake unafanywa kwa ushirikiano na Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara inatafiti na na kusambaza teknolojia rahisi za ufugaji wa samaki ili kuwezesha sekta binafsi kushiriki katika ufugaji wa samaki kwa kuongeza ajira, lishe na kipato nchini ikiwemo wananchi wanaoishi kwenye maeneo kame.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Serikali kupitia Ilani ya CCM ya 2015 – 2020, ahadi namba 25(d) iliwaahidi vijana wafugaji kuwa itatoa dhamana ya mikopo kwenye asasi za fedha.
(a) Je, Serikali imeandaa mkakati gani wa kuwawezesha vijana wafugaji kuunda vyama vya ushirika ili waweze kunufaika na ahadi hiyo ya CCM?
(b) Je, Serikali inayo orodha ya vikundi vya vijana wafugaji ambao wamejiunga na vyama vya ushirika ambao wameweza kunufaika na utaratibu wowote ulioandaliwa na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maria Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati ulioandaliwa na Serikali katika kuwawezesha vijana wafugaji kuunda vyama vya ushirika ni pamoja na kushirikisha Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvivi, Ofisi ya Rais TAMISEMI na wadau wengine katika kuhamasisha wafugaji, hususan vijana kuanzisha, kufufua na kujiunga na vyama vya ushirika vilivyopo. Uhamasishaji huo umefanyika kupitia mikutano na kampeni katika mikoa mbalimbali ikiwemo mikoa ya Tanga, Shinyanga, Mwanza, Iringa, Rukwa, Njombe, Manyara, Dodoma, Lindi na Mtwara ambapo wananchi walihamasika na kujiunga katika ushirika. Vilevile Wizara imeviunganisha vyama vya ushirika na wadau mbalimbali katika kuhamasisha ufugaji na uboreshaji wa mifugo. Baadhi ya wadau hao ni Oxfam, Care International na CARITAS.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ifuatayo ni idadi ya wafugaji waliohamashishwa kujiunga na vyama vya ushirika katika mikoa mbalimbali; Tanga jamii ya Wamasai na Wabarbaig wapatao 253; Njombe na Lindi wafugaji 265 walipatiwa elimu ya ushirika; Singida vikundi 62 vyenye wanachama 1,397 vilipatiwa elimu; Rukwa jumla ya wananchi 968 walihamasika kwa kujiunga kuanzisha vikundi vya ushirika; Dodoma kuna vikundi vipatavyo 338 ambavyo vinaundwa na rika mbalimbali; Shinyanga kuna vikundi 47, kati ya hivyo viwili vinajishughulisha na unenepeshaji wa ng’ombe na usindikaji wa ngozi. Taasisi za BRAC, Good Neighbourhood na World Vision zinatoa ufadhili wa mafunzo, ujenzi wa mabanda ya mfano, mifugo ya kuanzia kama mbegu pamoja na mashine za kuchakata ngozi kwa vikundi vya Mkoa wa Dodoma.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Serikali imeziagiza Halmashauri zote za Wilaya nchini kutenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya vijana na wanawake:-
Je, Serikali imetoa kiasi gani kwa vikundi vya vijana na wanawake tangu zoezi hilo lianze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka 2010 – 2016 Serikali imefanikiwa kutoa shilingi bilioni 122.4 kwa ajili ya mikopo ya vijana na wanawake ambazo zinatokana na asilimia kumi iliyotengwa kila mwaka kutokana na mapato ya ndani ya Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imepanga kutoa shilingi bilioni 56.8 ambapo mpaka mwezi Machi 2017 zimeshapelekwa shilingi bilioni 17.3 kwenye vikundi vya wanawake na vijana. Serikali itaendelea kutenga fedha hizo kila mwaka ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imeshatenga shilingi bilioni 61.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-
Kumekuwa na changamoto nyingi katika uvuvi wa Ziwa Victoria unaosababisha malalamiko mengi kutoka kwa wadau wa uvuvi.
Je, Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha inamaliza malalamiko hayo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uvuvi wa Ziwa Victoria umekuwa na changamoto nyingi zikiwemo shughuli za uvuvi haramu uliokithiri ambapo takribani asilimia 90 ya wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi hufanya vitendo vya uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo hivyo ni pamoja na kuvua kwa kutumia nyavu zilizounganishwa (vertical integration), kutumia nyavu za utali/timba (monofilament nets), kuvua kwa makokoro na nyavu zenye macho madogo chini ya kiwango kinachokubalika kisheria cha milimita nane na kadhalika. Aidha, uchakataji na biashara ya samaki wachanga na utoroshaji wa mazao ya uvuvi yakiwemo mabondo na kayobo kwenda nchi jirani bila kuzingatia sheria ni mojawapo ya vitendo vinavyoshawishi uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na vitendo hivyo, Serikali imedhamiria kulinda rasilimali za Taifa kwa kufanya Operesheni Sangara mwaka 2018 dhidi ya uvuvi haramu katika Ziwa Victoria. Operesheni hii ni kweli imeleta malalamiko kwa baadhi ya wadau wa uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kushughulikia malalamiko hayo, Serikali inaendelea kuhamasisha wavuvi, wafanyabiashara, watendaji wa Serikali na wadau wengine wote kufuata sheria na kanuni za uvuvi na kufanya mapitio ya Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 ili kuendana na mabadiliko ya sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imetoa elimu na inaendelea kutoa elimu kwa wadau wote kuhusu uvuvi endelevu. Pamoja na kufanya tafiti mbalimbali zinazosaidia wadau katika kuendeleza Sekta ya Uvuvi nchini katika kuchangia ukuaji wa uchumi wetu na wananchi wetu kwa ujumla. Tafiti hizo zinalenga kufanyika katika samaki wa maji ya asili na ukuzaji viumbe katika maji (aquaculture).
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kufanya tafiti zitakazopendekeza zana na njia sahihi za uvuvi zisizo na ahari katika uvunaji wa rasilimali za uvuvi. Pia kuimarisha vikundi vya ulinzi shirikishi wa rasilimali za uvuvi na kuandaa mwongozo wa kuvifanya vikundi hivyo kufanya kazi zake kwa ufanisi ili kutokomeza uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inatarajia kufanya semina kwa Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania kwa lengo la kutoa uelewa mpana kuhusu uvuvi haramu na jitihada zinazofanywa na Wizara yetu kupambana na uvuvi haramu kupitia operesheni zinazofanyika zikiwemo Operesheni Sangara, Jodari na ile ya MATT.
MHE. HAWA M. CHAKOMA (K.n.y. MARIA N. KANGOYE) aliuliza:-
Kumekuwa na malalamiko mengi juu ya matukio ya kikatili dhidi ya Watanzania wanaosafirishwa nje ya nchi na kufanyishwa kazi zisizo rasmi:- Je, Serikali imechukua hatua gani kudhibiti changamoto hii?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba Watanzania wanaopata fursa za kufanya kazi nje ya mipaka ya Tanzania wanafanya kazi katika mazingira mazuri na yanayolinda staha na utu wao. Hata hivyo, katika baadhi ya nyakati zimekuwepo taasisi ambazo kwa namna moja au nyingine zimekuwa zikitumia njia zisizo halali na kuwarubuni Watanzania kutofuata taratibu zilizopo za kupata ajira nje ya nchi. Kundi hili la wafanyakazi ndilo linalokumbana na kadhia ya kufanya kazi kwenye mazingira yasiyokuwa mazuri na hata matukio ya kikatili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ambayo Serikali imechukua ni kuweka utaratibu mzuri wa kutoa vibali kupitia mamlaka zinazoshughulikia masuala ya ajira ikiwemo Wakala wa Huduma za Ajira Tanzania (TAESA) iliyopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu na Kamisheni ya Kazi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Balozi zetu zilizopo nchi mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huo unaelekeza kila mfanyakazi kuwa na Wakala rasmi na kupata mkataba kutoka Ubalozini. Kwa utaratibu huo, Ubalozi unakuwa na taarifa katika kila hatua ambayo Watanzania wanapitia wakati wa maandalizi ya kwenda kufanya kazi, hivyo kusaidia kulinda maslahi yao. Aidha, mwajiri anayetaka kuajiri mfanyakazi kutoka Tanzania, atatakiwa kusoma na kuelewa mwongozo na baada ya kukubaliana nao, anatakiwa kujaza fomu ya kuomba kumwajiri Mtanzania na kuwasilisha Ubalozini kwa ajili ya kufanyiwa kazi. Maombi hayo yatafuatiwa na mkataba wa kazi ambao umetafsiriwa katika lugha ya Kiingereza na Kiarabu kwa nchi za kiarabu ili kurahisisha mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Watanzania ambao tayari walikuwa nje ya nchi bila kuwa na mikataba wala mawakala, Balozi zetu zimeanzisha utaratibu wa mikataba na alama za utambuzi ambazo zitatumika kwa ajili ya wafanyakazi ambao walikuwa nje ya nchi kabla ya kupata mikataba rasmi. Vilevile, katika kuhakikisha Watanzania waliopo nje wanakuwa salama katika maeneo wanayoishi, Wizara imeelekeza Balozi zetu zote kukusanya taarifa muhimu za Watanzania wanaoishi katika maeneo yao ya uwakilishi na kuwahamasisha kuwa na utaratibu wa kujiandikisha katika Ofisi za Ubalozi pamoja na Jumuiya mbalimbali za Watanzania walioanzisha katika nchi wanazoishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa rai kwa Watanzania wenye nia ya kufanya kazi nje ya mipaka ya Tanzania kufuata taratibu zilizowekwa na mamlaka husika kwa kuwa pamoja na mambo mengine inawapa kinga na kuepuka mazingira mabaya ya kazi yasiyotarajiwa na pia kurahisisha kupata msaada pale wanapohitajika.
MHE. HAWA M. CHAKOMA (K.n.y. MHE. MARIA N. KANGOYE) aliuliza:-
Kumekuwa na malalamiko mengi juu ya wananchi wanyonge hususani wanawake wajane na yatima kudhulumiwa ardhi hususani maeneo ya vijijini:-
Je, ni lini Serikali itaweka mikakati ya Kiwilaya ili kuwasaidia wananchi hao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikishughulikia migogoro ya ardhi vijijini katika ngazi mbalimbali kuanzia ngazi ya kijiji hadi ngazi ya Wizara. Migogoro inayopokelewa kutoka maeneo mbalimbali inahusu mirathi inayowagusa wajane na yatima katika maeneo ya vijijini, madai ya fidia ya fedha, viwanja/maeneo/mashamba, mwingiliano wa mipaka ya mashamba/viwanja, uvamizi wa wananchi katika maeneo ya taasisi za umma, taasisi kuingilia maeneo ya wananchi, migogoro baina ya wananchi na wawekezaji na migogoro ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali katika kuipatia ufumbuzi migogoro ya aina hiyo ni pamoja na kuanzisha Dawati Maalum la kusikiliza na kusaidia kutatua malalamiko ya ardhi yanayowasilishwa na wananchi. Dawati hilo pamoja na mambo mengine, linabainisha siku maalum za kupokea na kusikiliza malalamiko au kero hizo. Aidha, Serikali imeimarisha utendaji wa Mabaraza ya Ardhi ya Vijiji, Kata na Wilaya kwa kuelekeza kuwa uteuzi wa wajumbe wa Mabaraza hayo unakuwa wa uwiano sawia kwa kuzingatia uwepo wa uwakilishi wa wanawake.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuhimiza kuandaliwa kwa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji na wilaya (land use plans) ili kudhibiti mwingiliano wa matumizi ya ardhi. Aidha, ipo mikakati ya kurasimisha makazi kwenye vijiji na miji inayoondoa migogoro ya ardhi na kuinua kipato cha wananchi kwa kuwatayarishia hatimiliki ambazo hutumika kama dhamana katika kuomba mikopo kwenye taasisi za fedha.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya vituo vya Afya Mkoani Mwanza kukosa vyumba vya upasuaji:-

Je, ni nini mpango wa Serikali wa kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi kwa kucheleweshwa kufanyiwa upasuaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza una jumla vya vituo vya kutolea huduma za Afya vya Serikali 272 ikiwepo Hospitali sita, Vituo vya Afya 35 na Zahanati 231. Kwa sasa huduma ya upasuaji wa dharura kwa akina mama inatolewa kwenye Hospitali zote sita na Vituo 10 vya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupunguza vifo vinavyotokana na uchelewashwaji wa akina mama wakati wa kujifungua kwa kutokufanyiwa upasuaji, mwaka wa fedha 2017/2018 na 2018/2019 Serikali imepeleka kiasi cha shilingi bilioni sita kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa Vituo vya Afya 14 Mkoani Mwanza ambavyo kwa sasa viko katika hatua ya ukamilishaji na hivyo kuna Vituo 11 vya Afya ambavyo vilikuwa havitoi huduma za upasuaji, vitaanza kutoa huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilipeleka kiasi cha shilingi bilioni tatu Mkoani Mwanza kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya za Ilemela na Buchosa ambazo zitatoa huduma ya upasuaji wa dharura kwa akina mama, hivyo kutanua wigo na kuboresha huduma za upasuaji Mkoani Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kujenga vituo vya kutolea huduma za afya na kuongeza wataalam ili kumaliza tatizo la vifo vya akina mama vinavyotokana na uchelewashaji wa huduma ya upasuaji wakati wa kujifungua.
MHE. MARIA N. KANGOYE Aliuliza:-

Kumekuwa na mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kuelekea Mikoa ya Shinyanga na Tabora vyenye mitambo yake chanzo cha maji kule Ihelele Wilayani Misungwi, aidha maeneo yanayozunguka mitambo hiyo na yanayopitiwa na mabomba ya mradi huo hayana maji safi na salama.

Je, nini mpango wa Serikali kusambaza maji safi na salama kutoka Ziwa Victoria kwa wananchi wa vijiji vya Mkoa wa Mwanza hususan maeneo yanayopitiwa na bomba hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa maji kutoka Ziwa wa Victoria, Serikali ililenga kufikisha maji katika miji ya Kahama na Shinyanga na vijiji vyote vilivyopo kando ya bomba kuu la kusafisha maji. Kwa wakati huo vijiji vilivyokidhi na kuingizwa katika mradi huu vilikuwa ni vijiji vilivyopo umbali usiozidi kilometa tano kwa kila upande wa bomba kuu. Hivyo, jumla ya vijiji 39 vikiwemo vijiji vitano vya Mawile, Ilalambogo, Lubili, Isenengeja na Ibinza vya Wilaya ya Misungwi katika Mkoa wa Mwanza viliunganishwa na vilianza kupata huduma a maji tangu uendeshaji wa mradi ulipoanza mwezi Februari, 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo cha maji na mitambo ya kusafisha maji kwa mradi wa Kahama - Shinyanga iko katika kijiji cha Nyang’ohomango. Aidha, eneo hilo pia linapakana na vijiji vya Lubili, Isesa, Igenge na Mbalika. Kwa kutambua umuhimu wa maeneo haya kuwa na huduma ya majisafi na salama kwa mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilianza ujenzi wamradi wa maji vijiji vya Nyang’ohomango, Isesa, Igenge na Mbalika kwa gharama ya shilingi bilioni 6.1.

Aidha, fedha za kutekeleza mradi huu zinatolewa kwa asilimia mia moja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Inatarajiwa kuwa baada ya ujenzi huo kukamilika, jumla ya wananchi 14,606 wa vijiji hivyo na mifugo yao watanufaika na huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa mradi huu kutawezesha pia kuunganishwa kwa mradi wa maji unaoanzia kwenye kijiji cha Mbalika kwenda katika mji wa Misasi katika Wilaya ya Misungwi ambao pia utahudumia ziadi ya vijiji kumi.
MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-

Serikali iliahidi kuhamasisha sekta binafsi kuanzisha viwanda vikubwa na vya kati na kuweka utaratibu wa kuvilinda dhidi ya viwanda vya nje.

(a) Je, Serikali imefikia wapi katika zma hii ambayo ni mwelekeo wa kufikia uchumi wa kati na utoaji ajira hasa kwa vijana?

(b) Je, Serikali imeweka mkakati upi ili kuweza kujenga mazingira rafiki yatakayowezesha kupunguza gharama za uwekezaji na uendeshaji wa viwanda?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye Lyimo, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jukumu la Serikali kuhamasisha sekta binafsi kuanzisha viwanda vikubwa na vya kati ni la msingi na endelevu. Serikali imeendelea kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza katika viwanda kupitia kituo cha uwekezaji Tanzania yaani TIC na mamlaka ya kuendeleza maeneo huru ya uzalishaji kwa ajili ya kuuza nje yaani EPZA. Uhamasishaji huo unaambatana na kutoa vivutio mbalimbali ikiwemo misamaha ya kodi katika mitambo na mshine zinazotumika kwneye uzalishaji. Aidha, Shirika la kuhudumia viwanda vidogo vidogo (SIDO) limekuwa likihamasisha na kusaidia uanzishwaji wa viwanda vidogo na vya kati ambavyo ni msingi wa maendeleo ya viwanda vikubwa kupitia mafunzo na uwezeshaji wa kiufundi na mitaji.

Mheshimiwa Spika, pamoja na niliyoeleza katika swali namba 4404 lililojibiwa tarehe 07 Mei, 2019, ili kulinda viwanda vya ndani dhidi ya ushidani usio wa haki, Serikali kupitia Tume ya Ushindani (FCC) na Shirika la viwango Tanzania yaani TBS na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) vimekuwa vikidhibiti uingizaji wa bidhaa hafifu, bandia na zinazoingia kwa njia zisizo rasmi bila kulipiwa kodi. Vilevile Serikali imekuwa ikitoa misamaha ya kodi kwa baadhi ya bidhaa za ndani na kutozwa zaidi baadhi ya bidhaa zinazoingizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa mazingira bora ya biashara na uwekezaji ni kichocheo muhimu kwa maendeleo ya viwanda Nchini. Kwa kuzingatia umuhimu huo, Serikali imeendelea kutenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na biashara na kuyawekea miundombinu muhimu na kuanzisha kongano za viwanda yaani clusters ili kuwezesha wanaviwanda kupata huduma na kuendeleza viwanda vyao kwa urahisi.