Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Leah Jeremiah Komanya (2 total)

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziru Mkuu.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwambaSerikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya kazi kubwa katika sekta ya elimu na wananchi wameunga juhudi hizo kwa kuchangia ujenzi wa madarasa. Hata hivyo kuna maelfu ya wanafunzi waliofaulu kujiunga kidato cha kwanza hadi leo hawajaripoti shuleni kwaajili ya upungufu wa madarasa

Mheshimiwa Spika, nilitaka kujuwa ni nini kauli ya Serikali?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Komanya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sasa tunayo idadi nzuri na kubwa ya wanafunzi wanaofaulu darasa la saba kwenda Sekondari. Serikali msimamo wake ni kuwapeleka wanafunzi wote waliofaulu kwenda Sekondari kwa asilimia mia. Serikali imetoa maelekezo kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa kuhakikisha kwanza unafanya sense kupitia mfumo wa elimu ambao unaweza kuutabiri halmashauri hii inaweza kutoa wanafunzi wangapi kwenda Sekondari na kujipanga katika kuboresha katika miundombinu tayari kwa kuwapokea vijana hawa.

Kazi hiyo inafanywa kila halmashauri kwa usimamizi wake na wanapofaulu tunataka wote waende waanze kidato cha kwanza kwa wakati. Hata mwezi wa Disemba nilitoa kauli nikiwa mkoani Lindi kwamba kila halmashauri ihakikishe wanafunzi wote wanaenda awamu moja badala ya kuwaweka awamu mbili kwa sababu awamu mbili wale awamu ya pili wanakosa baadhi ya topics za kusoma na kwahiyo syllabus hawawezi kwenda pamoja; na kwamba kila Halmshauri isimamie hilo. Kwahiyo, usimamizi huu ni lazima uzingatiwe

Mheshimiwa Spika, na tumewapa deadline kufikia tarehe 31 mwezi huu wa kwanza wanafunzi wote wawe wamekwenda shule. Kwahiyo tufanye subira mpaka tarehe 31 tupate taarifa, inawezekana pia kuna wasiwasi wa awali, kwamba wanafunzi wengi hawajaenda lakini kutokana na maelekezo tuliyoyatoa, na muda tuliowapa mpaka tarehe 31 unaweza ukawa umekamilika; kwahiyo baada ya tarehe 31 tutatoa taarifa na swali lako litapata majibu mazuri. Kwa sasa msimamo wa serikali ni kuwapeleka wanafunzi wetu wote wanaosajiliwa. Awe anakwenda chekechea, anaingia darasa la kwanza, anaingia kidato cha kwanza, anaingia kidato cha tano, wote lazima waingie darasani kwa wakati na waanze kusoma kadiri syllabus inavyoeleza. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii muhimu. Kumekuwa na changamoto ya ukame kujirudiarudia nchini kwetu na matokeo yake ukame huu umeleta athari nyingi, ikiwemo mifugo kufa kwa kukosa malisho.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, Serikali ina mkakati gani wa muda wa kati na wa muda mrefu wa kukabiliana na ukame huu hususan kwenye malisho ya mifugo? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, amezungumzia ukame, anataka kujua mpango wa Serikali wa kukabiliana na ukame huu; ukame unaojitokeza mara nyingi nchini ni mabadiliko ya hali ya tabianchi ambayo yanaleta athari ya kukosekana kwa mvua na hasa pale ambapo athari hizo zinasababisha kutopata mvua kama ambavyo mwaka huu na mwaka uliopita hapa nchini kwetu, maeneo mengi yalikuwa makame kwa sababu hakuna mvua. Hii ni kutokana na mabadiliko ya tabianchi, lakini pia, ukame huu unatokana na uharibifu tu wa mazingira ambao wananchi wanaufanya kwenye maeneo yetu kwa kukata misitu na maeneo ambayo tunategemea sana kuwa na mvua.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, imeendelea kutoa elimu ya wananchi kuhifadhi mazingira kwenye maeneo yao ikiwemo misitu, ili isaidie kuleta mvua kwenye maeneo hayo kuachana na ukame. Hiyo ndio njia moja muhimu ambayo mimi naiona, lakini pia umehusisha maeneo ya malisho ya malisho ya mifugo. Kutokana na ukame huu ni kweli hatupati malisho na kwa hiyo, ni lazima pia tuhakikishe kwamba, tunaendelea kuhifadhi mazingira haya tupate mvua ili malisho mengi yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, ukiondoa ukame, lakini bado hata Wizara ya Mifugo na Uvuvi wanajitahidi sana kutoa elimu kwa wafugaji kuhakikisha kuwa wanafuga kitaalam kulingana na ukubwa wa malisho waliyonayo, ili kukabiliana na upungufu wa malisho ambayo kwa sasa yanakuwa hayapatikani kwa sababu ya kuwa na mifugo mingi zaidi. Jana tumelizungumza hapa ndani ya Bunge juu ya Ngorongoro kule, uharibifu unaoendelea kule Ngorongoro itakwisha, lakini hili ni sisi wenyewe ndio tutaweza kukabiliana nalo na kwa kuwa Serikali imeweka mkakati wa kuelimisha umma juu ya uhifadhi wa mazingira, lakini pia Wizara ya Mifugo inaendelea kuwaelimisha wafugaji, ili tuanze kuandaa malisho kwa kuhifadhi malisho, lakini pia tuweze kuchimba visima kupata maji ya chini na kuanza kumwagilia kwenye maeneo ambayo tumeyatenga kama maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake kwenye mifugo tumefanya jitihada kubwa sana za maeneo yetu yale ya ranch. Tumegawa vipande, vinaitwa blocks na kuwagawia wafugaji ili kila mmoja aweze kutunza maeneo hayo na ikiwezekana pia na kupanda nyasi ikiwa ni njia ya kupata malisho mapya, ili mifugo iweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito sasa kwa Watanzania, ili kukabiliana na ukame ambao unaendelea ni lazima tuungane pamoja turekebishe, tuache tabia ya kukata miti na misitu kwenye maeneo tuliyonayo ili misitu hii iweze kutusaidia kupata mvua za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe wito pia kwa ndugu zangu wafugaji waendelee kufuga kitaalam, tuwe na mifugo michache unayoweza kuihudumia ikiwemo kupata na malisho, ikiwezekana pia hata kuboresha malisho kwa mifugo uliyonayo badala ya kuwa ng’ombe zaidi ya 2,000 ambao hauna uwezo wa kuwafuga na matokeo yake kukosa malisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, huo ndio ujumbe wangu kwa swali ambalo Mheshimiwa Mbunge ameliuliza. Ahsante sana. (Makofi)