Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kiteto Zawadi Koshuma (32 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jina naitwa Kiteto Zawadi Koshuma, ni Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mwanza.
Mheshimiwa Spka, kwanza kabisa, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, japokuwa muda ni mdogo lakini nitachangia kwa kiasi fulani. Kwanza naomba niwashukuru wanawake wa Mkoa wa Mwanza ambao wameweza kuniamini ili kuwawakilisha katika Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba niongelee kuhusiana na hotuba ya Rais ambayo ilikuwa nzuri sana na imeweza kugusa nyoyo za Watanzania na kuweza kuwaonyesha Watanzania kwamba Tanzania sasa tunaweza tukawa na matumaini na Tanzania yetu na tukaishi kwa amani na mategemeo makubwa sana kutoka katika nchi ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hotuba ya Mheshimiwa Rais kabla sijaendelea ili muda usije ukaniishia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuongelea kuhusiana na mama lishe kitu ambacho kilimgusa sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, alipowaongelea mama lishe alisema Serikali sasa imefikia wakati iwatambue pamoja na shughuli zao wanazofanya. Mama lishe wamekuwa wakidharaulika sana, kama ambavyo Wabunge wengine wametangulia kusema.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikazie kwamba Waziri husika wa TAMISEMI atusaidie kwa kuwasiliana na Halmashauri zinazohusika ili ziweze kuwashirikisha kuhusu ni maeneo gani ambayo ni rafiki kwao kuweza kufanya shughuli zao za mama lishe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua mchango mkubwa ambao mama lishe wanao katika jamii yetu. Wengi wetu tunakula chakula kwa hawa mama lishe, lakini pia hawa mama lishe ambao wanatupatia chakula, wanajisaidia na wao kupata kipato, ambapo wanaweza wakatatua matatizo mbalimbali. Kama tunavyojua katika familia, mama pekee ndio mtu ambaye anajua kwamba watoto wamekula nini au baba amekula nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, naomba Serikali sasa ifikie hatua ya kuwatambua hawa mama lishe na kufahamu kazi ambazo wanazifanya kwamba zinachangia katika pato la Taifa na kukuza uchumi wa Taifa, hasa ukiangalia katika kauli mbiu ya Rais ambayo inasema Hapa Kazi Tu na sasa hivi ni kazi tu, hivyo tuwatambue hao mama lishe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais pia aliguswa sana tatizo la bodaboda. Bodaboda ni vijana wetu ambao, badala ya kutangatanga na kuwaibia watu kwenye mifuko yao wameamua kujiajiri kwa kupitia pikipiki ili waweze kujipatia kipato na hatimaye kutatua matatizo yao. Bodaboda hawa wamekuwa wakipata matatizo ya kuhamishwa kwenye vituo vyao ambavyo wanapaki kwa ajili ya kupata abiria.
Naiomba Serikali yangu ambayo ni sikivu, Serikali ya Chama cha Mapinduzi, iwasikilize hawa watu wa bodaboda, wawawekee vituo ambavyo na wao pia kwao ni rafiki ambapo wanaweza kupata abiria. Hii ni kwa sababu, nimegundua katika Halmashauri nyingi wanapangiwa vituo ambavyo siyo rafiki kwao. Boda boda hupangiwa sehemu ambayo hawezi kupata abiria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali yangu sikivu, itusaidie, mshuke kwenye Halmashauri ili muweze kuzishauri kwamba wanapotaka kuwapangia vituo hawa watu wa bodaboda, basi waweze kuwashirikisha ili wao pia wawepo katika kuchangia maamuzi kwamba ni wapi tukae ili kuweza kupata abiria na hivyo basi kuweza kusaidia katika shughuli zao mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nichangie upande wa viwanda suala ambalo Mheshimiwa Rais amelipa kipaumbele sana. Suala hili kama ambavyo wengi wametangulia kusema kwamba bila viwanda Tanzania haitaweza kuendelea, lakini sasa viwanda hivi vitaendeleaje kama hatutaweza kuwashirikisha watu ambao tayari wanahusika na viwanda?
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika Mkoa ninaotoka, Mkoa wa Mwanza ni Mkoa maarufu sana ambao samaki wa aina ya sato wanapatikana, lakini ni viwanda vichache sana ambavyo viko pale, kama vile Vic Fish, TFP na viwanda vingine lakini ni vichache sana.
Naiomba Serikali yangu inapokuwa inaleta mpango kazi wake, basi iangalie huu Mkoa wa Mwanza na kuufanya kuwa mkoa wenye viwanda. Kwa sababu gani nasema hivyo? Mwanza tunapata samaki…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa mzungumzaji)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie sentensi yangu. Pale Mwanza pia kuna Kiwanda cha Ngozi...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda tafadhali! (Kicheko)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/2017-2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa suala la Benki ya Wanawake Tanzania (TWB). Benki hii ilipoanzishwa mwaka 2009 lengo kuu ilikuwa kuwakomboa wanawake kiuchumi kupitia mikopo nafuu, kinyume na matarajio ya wanawake wote nchini, benki hii imekuwa ikitoa mikopo kwa riba kubwa sana, ya asilima kumi na tisa, riba hii imewafanya wanawake kushindwa kufanya biashara zao vizuri, kwa kuwa wanafanya biashara kwa kuhudumia mikopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeupitia vema Mpango huu wa Miaka Mitano, sijaona mwanamke akipewa kipaumbele, ukizingatia mwanamke hata katika jamii amekuwa mtu wa mwisho kuthaminiwa katika kipaumbele. Hivyo basi, naishauri Serikali, imwangalie mwanamke kwa jicho la tatu, hasa katika Mpango huu wa Maendeleo ya Taifa, ili kumwezesha kukabiliana na changamoto anazokutana nazo kama mwanamke katika jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali katika kipaumbele cha fedha katika Mpango huu, basi iongeze mtaji katika Benki ya Wanawake Tanzania (TWB), kwa kiwango cha shilingi bilioni thelathini, ili ifanye jumla ya mtaji wa benki hiyo, kuwa bilioni hamsini, kwani kwa sasa benki hiyo ina mtaji wa karibu bilioni ishirini.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, katika Mpango huu, katika suala la afya, Serikali imeweka mkakati wa kujenga blood bank mikoani. Mkoa wa Mwanza unayo blood bank katika hospitali teule ya Bugando, lakini wanawake wengi hupoteza maisha wakati wa kujifungua kwa kupungukiwa na damu. Hivyo basi, naishauri Serikali badala ya kujenga blood banks bora inunue majokofu ya kutunzia damu, katika kila Kata na kila Wilaya. Ili kusudi kila kituo cha afya na hospitali ya wilaya, iweze kujitunzia damu, kwa kuwa watu wengi Watanzania hupenda kujitolea damu. Hii itasaidia kupunguza vifo vya akinamama.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naishauri Serikali katika Mpango huu wa Maendelo ya Taifa, kwa kushirikiana na Wizara ya afya itenge fedha za kununulia CT scan katika kila hospitali ya Mkoa, ikiwemo hospitali ya Mkoa wa Mwanza ya Sekou Toure kwani wananchi hufa kwa magonjwa mbalimbali, ambayo kama kipimo cha CT scan kingekuwepo, mgonjwa angeweza kubainika ugonjwa unaomsumbua ili apatiwe matibabu sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja baada ya kuwasilisha ushauri wangu kwa njia hii ya maandishi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba nitumie nafasi hii kurekebisha jina langu naitwa Mheshimiwa Koshuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunipa nafasi ili na mimi niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu hususan katika Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusiana na suala la ubora wa elimu. Nimewasikiliza Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamekuwa wakichangia kuhusiana na ubora wa elimu kila mtu kwa kadri ambavyo ameweza na ni jambo zuri sana kwani kazi yetu sisi Wabunge ni kuishauri Serikali ili kuona kwamba watoto wetu wanapata elimu iliyo bora na sio bora elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende moja kwa moja upande wa vitabu na vitabu hivi vimegaiwa sasa kwa uwiano ambao mimi nauona kabisa kwamba hatuelekei kuzuri. Ukiangalia katika Mkoa wa Mwanza, Wilaya ya Ilemela, kwa mfano, darasa la pili wanafunzi ni 71,000 lakini vitabu ambavyo vimepelekwa katika Wilaya ya Ilemela ni vitabu 10,465. Wilaya ya Magu idadi ya wanafunzi wa darasa la pili ni 100,000 lakini vitabu ambavyo vimepelekwa ni 12,893 na hivyo ni vitabu vya hisabati. Wilaya ya Sengerema wako wanafunzi 151,000 na vitabu ambavyo vimepelekwa ni 13,965 na hivyo hivyo na Wilaya zingine. Waheshimiwa Wabunge kama mtapenda kuendana na mimi ni ukurasa wa 152 na 153.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ugawaji huu wa vitabu siamini kabisa kwamba wanafunzi wataweza kupata elimu iliyo bora. Kwa mfano, kwenye somo hili la hesabu vitabu ambavyo vimepelekwa ukiangalia idadi yake ni vichache ukilinganisha na idadi ya wanafunzi waliopo darasani wa darasa la pili. Hivyo, kwa mahesabu ya haraka haraka utakuta kitabu kimoja wana-share wanafunzi hata 30 hadi 40.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kujaribu kuwaeleza wazazi ukweli. Kutokana na hii Sera ya Elimu Bure ya mwaka 2016 wazazi wengi sasa wamekaa wanasema kwamba Serikali inatoa elimu bure wamesahau kwamba wao pia wanaweza wakachangia katika upatikanaji wa elimu nzuri ya watoto wao. Naomba niwashauri wazazi wote nchini kwamba na wao pia waweze kuisaidia Serikali, lakini pia na Serikali itusaidie sisi Wabunge kwa kupeleka elimu kwa wazazi kupitia Walimu Wakuu na Bodi za Shule wawasaidie kuwaeleza wazazi na wao pia wasaidie kuchangia. Kwani wazazi wakichangia vitabu watasaidia watoto walau kila mmoja kuwa na kitabu chake kama inawezekana au kitabu kimoja kutumiwa na wanafunzi hata watatu hadi watano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shule nyingi ambazo zinafanya vizuri hapa nchini Tanzania hususan shule za msingi katika elimu ya darasa la kwanza mpaka la saba ni shule za private lakini shule za Serikali zimekuwa ziki-lag behind. Kuna sababu nyingi tu ambazo zinazosababisha shule za Serikali kutokufanya vizuri zikizidiwa na shule zile za private.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kabisa wazi kwamba mimi ni mmiliki wa shule za private, lakini ukiangalia katika shule za private tunaletewa miongozo mingi sana na mnaambiwa kitabu kimoja kitumiwe na wanafunzi watatu. Kwa kweli shule za private zimekuwa zikijitahidi sana kuzingatia hilo na ndiyo maana wanaofaulu kwa ufaulu mkubwa wanatoka katika shule za private. Naomba Serikali sasa iweke mkazo katika shule zetu, ndio tumetoa elimu bure lakini sasa kama vitabu vinakuwa ni vichache wanafunzi hawawezi kupata elimu iliyo bora wanatapa bora elimu na kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni upungufu wa madarasa na miundombinu mingine. Ukiangalia mwaka kwa 2015/2016 uandikishwaji wa wanafunzi mashuleni uliongezeka kwa asilimia kubwa sana. Hiyo ni kutokana na sera nzuri ambayo imetengenezwa na Serikali yetu, Sera ya Elimu Bure. Sasa miundombinu bado ipo ile ile ambapo zamani wazazi walikuwa wanaogopa kupeleka watoto shuleni, madarasa ni machache, wanafunzi hawatoshei kwenye darasa yaani unakuta darasa moja wanakaa wanafunzi zaidi ya 100, mwalimu ni mmoja na wengine bado wanakaa chini. Kuna shule ambazo mpaka leo bado wanafunzi wanakaa chini. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais amesisitiza suala la kuwa na madawati na akasema Wakuu wa Wilaya ambao hawatawajibika katika shule zao kuhakikisha kwamba madawati yanapatikana watafukuzwa kazi lakini bado kuna shule zingine bado wanafunzi wanakaa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote mimi nachosema na mawazo yangu ambayo nafikiria, ni afadhali wanafunzi wakae chini, lakini wale wanafunzi wakapata walimu wa kuwafundisha na madarasa yakatosha. Walau basi tufanye kama ambavyo shule za private zinafanya, unakuta darasa moja la kwanza linakuwa na wanafunzi labda 45 kwenye shule za private na hiyo yote ni kutokana na kwamba tunafuata vizuri miongozo inayotolewa na Serikali kwa shule za private lakini kwenye shule za Serikali unakuta darasa moja wapo wanafunzi 100 hadi 120.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imejitokeza sehemu nyingi sana kama ningesema nitoe mifano nina mifano mingi hata kwa shule za mjini. Kwa mfano, kuna shule moja ipo pale Mwanza, Wilaya ya Ilemela inaitwa shule ya Isenga, darasa la kwanza mpaka la tatu wanafunzi 120 darasani. Naomba Serikali ijitahidi sana kuweza kuwekeza katika kuongeza madarasa ili wanafunzi wawe wachache na hata kama mwalimu atakuwa mmoja katika darasa ambalo lina wanafunzi wachache tunaamini kabisa wanafunzi hao wataweza kujua kusoma, kuandika na kuhesabu. Kwa sababu tunaona unapoweka idadi ndogo ya wanafunzi na mwalimu akawa anaweza kumpitia kila mwanafunzi moja mmoja darasani basi wanafunzi hao wataondoka pale wakijua kusoma, kuandika na kuhesabu na hivyo kuelekea kwenye upatikanaji wa elimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu bado utaendelea kwenye upatikanaji wa elimu bora na sasa nizungumzie kuhusu motisha za walimu. Walimu wanapokosa motisha kwa kweli inawa-demoralize. Unakuta walimu wanakuwa hawana moyo wa kufundisha kwa sababu hawapati motisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Serikali ilikuja na mpango mzuri sana wa Big Results Now na uliwasaidia walimu wakawa wanafanya kazi kwa kujitoa wakiamini kwamba mwisho wa siku watapewa motisha. Sasa mpango huu umeenda unalegalega tu. Naomba Wizara ya Elimu warudishe mpango huu wa Big Results Now na kuuwekea mkazo ili uweze kusaidia walimu kufundisha wanafunzi vizuri na hatimaye kutoa elimu iliyo bora ili waweze kupewa motisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la hardship allowance. Wameongea Waheshimiwa wengi sana kuhusiana na maslahi ya walimu, unakuta mwalimu anatolewa kituo kimoja kupelekwa kituo kingine na anapelekwa kule ni kijijini, lakini anapofika kule anakuta hakuna nyumba, kama kuna nyumba hakuna umeme, hakuna choo yaani unakuta mazingira ni magumu kiasi kwamba huyu mwalimu hawezi kuwa na moyo hata wa kuingia darasani. Inampasa huyu mwalimu asubuhi akiamka atume wanafunzi kwenda kuteka maji kwa ajili yake. Hivi kweli tunategemea hapo tutapata wanafunzi ambao wanajua kusoma na kuandika, tutawapata wapi wakati wanafunzi hao wanatumika kwenda kuchota maji? Naomba sasa Serikali isaidie kutoa hardship allowance kwa walimu ambao wanapelekwa katika mazingira magumu ili waweze kupata moyo wa kufundisha wanafunzi wetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la kubadilika kwa mitaala, hiyo yote pia inapelekea kwenye kupata elimu iliyo bora. Mitaala imekuwa ikibadilika mara kwa mara, anapokuja Waziri huyu anabadilisha mfumo wa elimu na mitaala, anapokuja Waziri mwingine anabadilisha mfumo wa elimu na mitaala, suala hili linawachanganya wanafunzi. Siyo tu kuwachanganya wanafunzi bali wananchi pia wanabaki wamechanganyikiwa hawajielewi hivi wafuate mfumo au mtaala upi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mitaala inapokuwa inabadilika vitabu pia inabidi vibadilishwe. Kwa hiyo, naiomba Serikali inapobadilisha mitaala vitabu viende kwa haraka sana. Kwa mfano, mwaka huu vitabu vimechelewa sana kwenda ndio kwanza vimetoka juzi tu vimesambazwa, vimechelewa sana tayari walimu walikuwa wanatumia vitabu vya zamani, wanashindwa jinsi ya wakuwafundisha wanafunzi... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Koshuma.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Wizara ya Katiba na Sheria.
Pili, naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia fursa hii ili niweze pia kuendelea kuchangia katika Hotuba hii ya Wizara ya Katiba na Sheria. Ninawashukuru pia wanawake wa Mkoa wa Mwanza ambao waliniamini na kunipa kura nyingi na kuweza kuwawakilisha katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ninaomba kuchangia kwa upande wa Sheria ya Ndoa. Katika Sheria ya Ndoa nimeangalia na kuona kwamba kuna upungufu ambao unafanya sheria hii kukandamiza haki za wanawake katika Sheria ya Ndoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kuna contradictions ambazo zinatokea katika Sheria ya Ndoa. Mtoto wa kike katika sheria hii anaweza akaolewa akiwa na umri wa miaka 16 lakini ukija katika Sheria ya Watoto (Children Act Law) mtoto anajulikana ni mtoto mwenye umri wa kuanzia sifuri hadi miaka 18, lakini kuna sheria ya Sexual Offensive Act, sheria hii pia na yenyewe inakuambia kwamba mtu ambaye anafanya mapenzi na mtoto mwenye umri chini ya miaka 18 amefanya kosa la jinai. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapata wakati mgumu sana kwamba hizi sheria tatu ambazo nimeziangalia zinaleta contradictions na zinamgusa mtoto wa kike, kwa sababu mimi ni mwakilishi wa wanawake siyo tu wa Mkoa wa Mwanza bali ni mwakilishi wa wanawake Tanzania nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, inaniuma sana kuona kwamba mtoto mdogo, tayari umemuita ni mtoto katika Children Act Law, mtoto ni wa umri chini ya miaka 18 lakini kwenye Sheria ya Ndoa unampa mwanaume mamlaka ya kumchukua huyu mtoto asiyekuwa na hatia, ambaye psychologically akili yake bado haijaweza kufikiria lolote kuhusiana na suala zima la ndoa. Lakini umempa mamlaka mwanaume aweze kumchukua mtoto huyu na kumweka unyumba kitu ambacho naona ni unyanyasaji kwa mtoto wa kike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, ninaitaka Serikali itakapokuja kujibu hoja za hotuba yake basi ije na kauli moja, kwamba inasema nini kuhusiana na hizi contradictions ambazo zinatokea katika hizo sheria tatu ambazo nimeziainisha hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusiana na kesi kurundikana katika mahakama zetu. Kesi zimekuwa ni nyingi sana zinarudikana kwenye mahakama na kufanya mahabusu kuwa wengi kwenye mahakama zetu. Lakini ukiangalia katika kesi hizo siyo wote wanaoenda kushtakiwa mahakamani wana makosa, wengi wao wamekuwa wakibambikwa kesi. Mfano mtu kaiba kuku lakini kwa sababu kuna fisadi mmoja ambaye amejificha somewhere anataka kumtumia huyu mtu ambaye ameiba kuku tu basi ahukumiwe kwa kesi ya kuiba kuku, lakini mtu huyu anapewa kesi ya mauaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inasikitisha sana unajiuliza Taifa letu la Tanzania tunaelekea wapi. Kwa uchungu mkubwa sana ninaiomba Serikali ianze kuangalia kesi hizi, japokuwa kwa juhudi za Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli amelikemea sana suala hili la kesi kurundikana mahakamani hadi akaweza kuwaongezea Majaji fedha kwa ajili ya kuweza kuendesha kesi, lakini bado kesi zinaendelea kurundikana mahakamani na kesi nyingi kwa kweli ni zile za kusakiziwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naiomba Serikali itoe tamko kwa vyombo hivi vya kisheria ambavyo vinasimamia reinforcement ya sheria kwamba ni nini kinatakiwa kifanyike kwenye kesi ambazo ziko mahakamani ili kuweza kupunguza watuhumiwa hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ni kuhusiana na utoaji wa haki na utawala wa sheria. Kwa masikitiko makubwa sana na hata kama ni kulia ningeweza kulia mbele ya Bunge lako Tukufu, wanawake wamekuwa wakinyanyasika sana, mwanamke utakuta amepigwa na mume wake, anakwenda kushtaki polisi mwanaume anapelekwa mahakamani, lakini bado mwanamke huyu anaoneka kwamba ilikuwa ni halali kwa mwanaume kumpiga huyu mwanamke kana kwamba ni ngoma yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali ijaribu kuangalia suala zima la wanawake kunyanyasika katika utoaji wa haki zao. Unakuta kwa mfano, hapa sijui ni sheria gani inahusika lakini unakuta mwanamke ameolewa na mume wake kwa ridhaa yake na wanaishi vizuri, baada ya muda mfupi mwanamke huyu na mwanaume wanaamua kutengana kwa sababu labda wametofautiana baadhi ya vitu. Katika utofauti huo basi unakuta mwanaume anapofika Mahakamani kwa ajili ya kutoa talaka, mwanamke huyo anapopewa talaka anaambiwa nenda halafu mali zote anaachiwa mwanaume.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inasikitisha sana kwa sababu ni wanawake wengi sana afadhali hata wale ambao wamejaliwa basi hata kusoma wamepata elimu wanajua ni jinsi gani wataweza kujikwamua kuondokana na unyanyasaji huu ambao tunaupata kutoka kwa wanaume. Lakini vipi wale kundi kubwa la wanawake ambao hawajakwenda shule? Hawajui ni nini wafanye?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali kwa kushirikiana na Wizara husika waweze kuangalia dawati la kijinsia ambalo lipo lakini kiuhalisia halina kazi linayofanya. Ninaitaka Serikali sasa ianze kuangalia masuala ya kusaidia utoaji wa haki kwa wanawake na kuhakikisha kwamba wanawake wote wanapatiwa haki zao. Kwa sababu wanawake wengi wamekuwa wakinyimwa haki zao hata pale wanapofiwa na waume zao. Wajane wameteseka, wamenyang‘anywa mali na kuondoka bila chochote, wanabaki wanahagaika mtaani wakati ndugu wamebeba mali zote wameondoka wanajisifia mtaani kwamba wanazo mali halafu mwanamke huyu anaanza kukanda maandazi, anauza karanga, anafunga ufuta ili mradi maisha yake yaweze kusogea. Inasikitisha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kuongelea kuhusiana na kesi za Serikali. Inasikitisha kwamba Serikali inakuwa na kesi nyingi sana, inashitaki watu kwa kufanya makosa, lakini kesi zote almost 99 percent ya kesi za Serikali inapoteza ama Serikali inashindwa. Ninaitaka Wizara ije iseme, itoe tamko lake kwamba kwa nini Serikali inapoteza kesi nyingi? Ni kwa sababu gani kesi ziwe nyingi Serikali inashindwa? Kesi 1000 Serikali inashinda kesi mbili tu, inasikitisha sana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumalizia kwa kuongelea kuhusiana na suala zima la majengo ya mahakama ambayo yamechakaa sana. Naomba Serikali katika bajeti yake iangalie ni namna gani itaweza kusaidia kufanya renovation ya majengo ya mahakama Tanzania nzima kwa sababu ya kuweza kuwasaidia wananchi kupata haki zao lakini pia kuongeza watumishi katika Mahakama zetu. Kwa sababu upungufu wa watumishi ume-deprive haki za wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nimalizie kwa kukushukuru sana na kumshukuru Mungu kwa sababu ya kutoa speech hii ahsante sana. Naunga hoja mkono ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu katika kujadili bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kunijalia afya njema, uwezo na hekima katika kujadili majadiliano mbalimbali katika Bunge hili. Leo hii napenda sana nimuombe Mwenyezi Mungu anijalie hekima ili niendelee kuishauri Serikali yangu ambayo ni sikivu na naamini kabisa kwamba watanielewa na kufanyia kazi maoni yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuanza, naomba kidogo nikosoe jambo moja. Kuna Mbunge amemaliza kuchangia akasema kwamba Serikali ya CCM ni wezi, lakini katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 8 inaonesha ni jinsi gani Serikali inavyomilikiwa na wananchi kwa maana kwamba watendaji wanafanya kazi kwa niaba ya wananchi. Kwa hiyo, itakuwa si sahihi nikiendelea kuruhusu Mbunge mmoja kusema kwamba Serikali ya CCM ni wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba jambo hilo ambalo yule Mbunge ametoka kuchangia akasema Serikali ni wezi liweze kufutwa kwenye Hansard. Kwa sababu Wana-CCM siyo wezi na ndiyo maana mara kwa mara Serikali ya CCM imekuwa ikijikosoa pale ambapo inaona imekosea, bali ni mtendaji mmojammoja ndiye anayekosea, hivyo huwezi ukasema kwa kutumia ule msemo kwamba samaki mmoja akioza wameoza wote, anashughulikiwa mtendaji mmojammoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, naomba tena niende katika kipengele kingine cha kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Ninayo furaha kubwa sana kwa siku ya leo kumpongeza Rais wetu. Kwa sababu gani ninampongeza Rais wetu? Rais huyu ni fahari ya Watanzania, ni fahari ya Wanachama wa Chama cha Mapinduzi, ni fahari ya mataifa mbalimbali na ni fahari kwa dunia nzima. Mambo ambayo anayafanya Mheshimiwa Rais Dokta Magufuli anastahili kupewa pongezi yeye kama yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mbunge siku moja alidiriki kusema kwamba Mheshimiwa Magufuli alisema ni Serikali ya Dkt. Magufuli, hapana, siyo kwamba alisema chagua Serikali ya Magufuli bali alitaka tumuamini yeye kama mtu lakini si kwamba Serikali ni ya kwake, Serikali inamilikiwa…

TAARIFA....

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Mheshimiwa Bwege kwa kweli siwezi kuikubali na ndiyo maana nilianza kwa utangulizi wa kuongelea Ibara ya 8 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lowassa alikuwa ni mtendaji na atawajibika kama mtendaji. Mimi sitaki kuyahesabu yaliyopita, nasonga mbele na haya tuliyonayo sasa hivi. Ndiyo maana nikasema siku ya leo naomba Mungu aendelee kunipa hekima na naendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema, kwanza naomba unilindie dakika zangu kwa sababu nilizitenga kwa makundi, Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli sisi wana CCM tunayo kila sababu ya kujivunia. Hata mimi mwenyewe naposimama hapa siku ya leo nasimama najidai kwa sababu tumemchagua Rais, tukamnadi sisi wenyewe, tukatembea kijiji kwa kijiji, nyumba kwa nyumba, shuka kwa shuka tukitafuta kura za Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Leo hii siwezi kuona aibu kuivaa nguo ya kijani kutembea barabarani kumuongelea Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa sababu mambo anayoyafanya naamini kabisa hakuna Mtanzania ambaye angeweza kuthubutu, mambo aliyoyafanya ni ya msingi sana na ni mazito na yanawagusa wanyonge. Ndiyo maana katika michango yangu ndani ya Bunge hili nimekuwa nikimtaja Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwamba ni Rais ambaye yuko tayari kuwatumikia wanyonge na napoona kuna kitu ambacho kinawakandamiza wanyonge nimekuwa nikijaribu kuishauri Serikali yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kurudi katika michango ya bajeti. Naomba kuchangia suala la Deni la Taifa. Katika kitabu chake Waziri wa Fedha na Mipango ameongelea suala zima la ustahimilivu wa Deni la Taifa. Mimi sipingani na hilo lakini nachokisema ni kwamba Deni la Taifa kama ni stahimilivu waendelee kukopa lakini Deni la Taifa linapokuwa linaongezeka halafu Watanzania wanaendelea kuishi katika maisha ya umaskini, tunaona hakuna sababu ya kukopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali jambo moja, tunapokopa na tunapoendelea kuongeza Deni la Taifa kama anavyosema kwamba bado ni stahimilivu, liende likawekezwe kwenye miradi ambayo inaweza ikawasaidia Watanzania. Kwa mfano, kuna matatizo ya maji mpaka leo kila Mbunge akisimama humu ndani analalamikia suala la maji katika jimbo lake, Mkoa wake na Wilaya yake. Sasa najiuliza swali, hivi Deni hili la Taifa ambalo linaongezeka siku hadi siku halafu wananchi bado wanaendelea kulia na maji, mnasema kwamba tunamtua mwanamke ndoo kichwani lakini katika hili bado hatujafaulu. Naomba niendelee kuishauri Serikali iweze kuzingatia mambo haya ya kurekebisha masuala mazima ya miradi ya maji. Kuna miradi mingi sana ambayo inaanzishwa lakini haikamiliki. Kwa hiyo, utaona ni jinsi gani Deni hili la Taifa bado halijawa la kuwanufaisha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kidogo Mkoa wa Mwanza. Kwa mfano, kuna mradi mkubwa wa maji kule Ilemela ambao ulikuwa unafadhiliwa na World Bank, mradi huu ulikuwa ni wa vijiji kumi lakini katika hivi ni kijiji kimoja tu cha Kayeze ambacho ndiyo kimepata maji, lakini vijiji vingine kama vile Nyafula, Kasabangu, Nyamadoke, Kabangaja, Sangabuye na kwingineko kote huko bado hawana maji. Ukiangalia pale Mwanza tumezungukwa na Ziwa Victoria, fikiria wale tu ambao wanaishi kandokando ya Ziwa Victoria wanaenda kuchota maji machafu ina maana Serikali imeshindwa kuwasogezea maji katika nyumba zao. Naomba sana Serikali iliangalie suala la usambazaji wa maji katika vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika mradi ambao unatokea Misungwi kuelekea Kahama na Shinyanga umeviacha vijiji vya Nyangomango, Ilambogo na Ibinza. Siku moja Mheshimiwa Mbunge wa Misungwi hapa aliongea kwa uchungu sana na watu hawakumuelewa lakini mimi nilimuelewa kwa sababu nimepita katika vijiji vile na nikaona tatizo lililoko pale. Hatutaweza kuvumilia hali hii ambapo miradi ya maji inapita halafu inaviacha vijiji vile vya kandokando pale vyote havina maji halafu mnaona maji yanapita kutoka Ziwa Victoria yakienda sehemu nyingine halafu vile vijiji vinakosa maji. Naomba sana Serikali iweze kujirekebisha katika suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia upande wa Sengerema kuna mradi mkubwa ambao unatakiwa kusambaza maji lakini bado kuna vijiji ambavyo havina maji, kwa mfano Kijiji cha Kwang’washi na chenyewe hakina maji, wananchi kila siku wanalia, akina mama wanaamka wanatembea kilometa zaidi ya 20 kwenda kutafuta maji. Kwa kweli kama tuko tayari kusaidia wananchi wetu ambao ni wanyonge, hebu tuwasaidie katika kutatua matatizo yao ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu sijaona suala la kilimo. Kama tunavyofahamu asilimia 75 ya Pato la Taifa inachangiwa na kilimo. Sioni ni kwa sababu gani tunashindwa ku-link bajeti kuu ya Serikali na suala zima la Kilimo. Naomba Waziri wa Fedha na Mipango atakaposimama atueleze sisi Waheshimiwa Wabunge suala la kilimo analiweka vipi, tunaelekea wapi, kwa sababu kama tunaenda kwenye uchumi wa kati au uchumi wa viwanda tutafikaje kwenye uchumi wa viwanda wakati kilimo hakitiliwi maanani. Naomba sana Serikali iweze kutilia maanani suala la kilimo kwa sababu kilimo kitaweza kusaidia wananchi wengi kuajiriwa kwenye mashamba lakini hatimaye pia kuondokana na suala zima la njaa, kwa sababu tunaona vijiji vingine wanakufa na njaa na hili hatuwezi kuacha kulisemea kwa sababu wananchi hawatatuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee hali ya uchumi. Kwa masikitiko makubwa sana nilipokuwa nikisoma kitabu cha fedha na mipango, Waziri anasema kwamba hali ya uchumi ni nzuri. Kusema ukweli hali ya uchumi si shwari, hali ya uchumi ni mbaya sana, wananchi wanaishi maisha ya kimaskini, hata hajui kama atapata hata mlo mmoja, si tu milo miwili au mitatu, hajui hata kama atapata mlo mmoja. Naomba Serikali inapokuwa inaandika vitu ijaribu kuangalia maisha ya Watanzania kwanza yako vipi. Inawezekana wataalamu ambao wanaandika hivi vitabu wao wana maisha mazuri, kwa hiyo, hawafikirii wale Watanzania ambao wana maisha mabaya, ambao maisha yao hayako katika hali nzuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niendelee kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu lakini niendelee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunijalia afya njema ili niendelee kutoa michango yangu katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara ya Fedha ninaomba nianze kwa kuchangia suala la ukusanyaji wa mapato. Ni jambo ambalo nimekuwa nikilifikiria sana pamoja na kulifikiria hata Mheshimiwa Rais amewahi kuliongelea katika kampeni zake na hata wakati wa kufungua Bunge hili. Suala hilo ni suala la wafanyabiashara kuombwa kulipa kodi wakati hata biashara yenyewe hajaianza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo imani kubwa sana kwamba Wizara ya Fedha ndiyo Wizara ambayo inahusika kwa kiasi kikubwa sana kwa sababu makusanyo haya ya mapato ya kodi yanakusanywa na TRA. Mfanyabiashara kama hajaanza biashara yake amechukua mtaji wake, anaanza biashara, maana yake ni kwamba anaanza kwanza kwa kulipia kama ni chumba cha kufanyia biashara, pili anaweka bidhaa anazotaka kuziuza. Sasa kama mfanyabiashara huyu unaanza kumwambia kwamba alipe kodi kwanza ndipo aendelee na biashara yake ina maana pesa hiyo anaitoa kutoka kwenye mfuko wake ambao ndio mtaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi ninaona kabisa suala hili ni kuwadhulumu wafanyabiashara na sio tu kuwadhulumu bali ni kuwafanya wafanyabiashara wasiwe na moyo wa kulipa kodi. Ndio maana unakuta hapa Tanzania unaona watu hawana moyo wa kulipa kodi. Sio kwamba wafanyabiashara hawataki kulipa kodi, wanapenda sana kulipa kodi lakini kama mtu unataka kuanza biashara unaenda kuomba leseni kwenye Halmashauri, Halmashauri wanakwambia hatuwezi kukupa leseni pamoja na kwamba umejaza fomu mpaka utuletee tax clearance. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili linawaumiza sana Watanzania na mimi sitapenda kuona watanzania wakiendelea kuumia kwa sababu wanaoumia ni wafanyabiashara wale ambao ni wadogo wadogo ambao pesa zao wanazipata kwa taabu sana, halafu anapokuwa amepata mtaji wake ili aanzishe biashara Serikali na yenyewe inasogea inaanza kumwambia lipa kwanza kodi ndio uende kufanya biashara. Kwa akili tu za kawaida, hata hazihitaji uende darasani, hivi unawezaje mtu ukaanza kulipa kodi kabla hata biashara yenyewe hujaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kubwa sana kwamba nikifungua biashara yangu nikaanza kuifanya ndipo mtu aniijie aniambie lipa kodi, kwa sababu moja kwa moja nitakuwa nimejua baada ya zile administration cost na operation cost, sasa faida yangu ni kiasi gani. Kwa hiyo, hata ukija kuniuliza mapato yangu ninayajua kwa kichwa kwa sababu tayari nimeianza biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri sana Serikali iweze kuangalia na kutekeleza kwa sababu hili ni agizo la Mheshimiwa Rais. Wakati Mheshimiwa Rais anazunguka kwenye kampeni yake, alikuwa anaongea kwa uchungu sana na mimi namwamini sana Mheshimiwa Rais nikiamini yeye anayo nia ya kuwasaidia watanzania ambao ni wa hali ya chini, namwamini sana Mheshimiwa Rais. Sasa sisi watendaji ambao tunamsaidia Mheshimiwa Rais hatupo tayari kumsaidia kwa sababu yale anayoyasema hatuyaweki kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Wizara hii, Mheshimiwa Waziri wa Fedha uweze kufanyia kazi masuala ya TRA kuanza kukusanya kodi wakati mfanyabiashara bado hajaanza kufanya biashara yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nisemee kuhusu suala la shilingi milioni 50 katika kila Kijiji. Sitawahi kukaa ninyamaze hata siku moja kwa sababu mimi ni mwakilishi wa wanawake na kila siku nimekuwa nikisema mimi ni mwakilishi wa wanawake sio tu Mkoa wa Mwanza bali Tanzania nzima. Shilingi milioni 50 katika kila kijiji ipo katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Waziri wa Fedha ameeleza kabisa mwanzo kabisa wa ukurasa wake kwamba anatengeneza bajeti hii kutokana na mambo mengi tu lakini Ilani ya Chama cha Mapinduzi ndio ambayo inamuelekeza ni namna gani aweze kutekeleza bajeti yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la shilingi milioni 50 kila kijiji sielewi nianzie wapi, nikiangalia katika kitabu hiki cha Waziri sijaona ni sehemu gani inaonekana shilingi milioni 50 kila kijiji itatoka. Mwaka jana nilisimama hapa hapa Bungeni kwa kutumia kitabu hiki cha Wizara ya Fedha cha mwaka 2016/2017 shilingi milioni 50 katika kila kijiji ilikuwepo, ilikuwa imetengwa. Nashukuru kwamba Kamati imeweza kutusaidia kutuonyesha kwamba katika mwaka wa fedha 2016/2017 shilingi milioni 50 kila kijiji ilikuwa imetengwa shilingi bilioni 59 na kwa mwaka huu wa fedha Kamati imetuambia kwamba katika ukurasa wake wa 20, Kamati inaeleza kabisa wazi pale kwamba shilingi bilioni 59, zilizotengwa 2016/2017 bado hazijatoka lakini kwa sasa Kamati imeeleza kwamba shilingi bilioni 60 sasa imetengwa kwa ajili ya kutekeleza suala la shilingi milioni 50 katika kila kijiji.

Nashangaa sana Mheshimiwa Mbunge sijui anataka kunipa taarifa gani, sijamuelewa, kwa sababu gani, suala ninaloliongea lipo katika kitabu hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo mimi najitahidi kuhoji hapa ni kwamba kwa nini kamati imeeleza kwamba shilingi bilioni 60 imetengwa katika mwaka huu wa fedha 2017/2018, lakini katika kitabu chake cha Wizara shilingi bilioni 60 siioni. Kwa hiyo, naomba atakapokuja kusimama pale kuhitimisha hoja yake Mheshimiwa Waziri aweze kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba hii shilingi bilioni 60 ambayo Kamati ya Bajeti inaiongelea kwenye kitabu chake ipo ukurasa wa ngapi, aweze kutuelezea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla muda wangu haujaisha ninaomba niseme kwamba pamoja na kwamba hii shilingi milioni 50 kila kijiji imeelekezwa, lakini hizi fedha kama tutakuwa tunazitenga kila mwaka halafu haziendi, ninaiomba Serikali wakati wanakuja kuhitimisha watueleze ni lini itaanza kwenda. Tumekuwa tukijibiwa humu majibu, Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiuliza maswali mara kwa mara na kujibiwa kwamba fedha hizi zitaanza kupelekwa pale ambapo utaratibu utakuwa umekamilika wa kupeleka fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi sasa hivi ukiniuliza tuanze na mradi gani, tupeleke katika vijiji gani, tupeleke katika Mikoa gani, ninaweza nikaisaidia Wizara ya Fedha. Hii ni kwa sababu mwaka jana wakati tunajadili hapa bajeti kuna mikoa ilitajwa kwamba ni Mikoa maskini, ikiwemo Kagera na Kigoma. Tunaomba Wizara hii ilipokuwa imeeleza mwaka jana kwamba wataanza na mikoa mitatu ambayo itakuwa ni mikoa ya pilot study, tunaomba basi hiyo mikoa mitatu watuambie ni Mikoa gani na kama wameshapeleka watueleze ni Wilaya zipi na kama wameshapeleka watueleze vijiji gani ambavyo vimepata pesa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaamini kwamba Watanzania watakuwa wamesikia ni kwa namna gani nimeweza kuwawakilisha katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tena niweze kuongelea suala la allocation ya bajeti, naamini Wizara hii ndiyo inahusika katika kuandaa bajeti, katika kuweka allocation ya resources. Suala la allocation ya bajeti naomba iwe inaangalia zile Wizara ambazo zinagusa moja kwa moja maisha ya Watanzania. Naomba niishauri Serikali inapokuwa inaweka allocation ya bajeti, iangalie Wizara ya Maji.Wizara ya Maji iwekewe fedha za kutosha.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini kabisa Wizara ya Maji ikiwekewa fedha za kutosha wananchi wakipata maji wataweza kulima, baada ya kulima ndipo tutaweza kuanza kuongelea viwanda. Hatuwezi tukaanza kusema viwanda wakati hata kilimo hatukioni. Kilimo hakina dira kabisa, hatuwezi kulima kwenye ardhi ambayo ina ukame… (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini unapokuwa Mbunge, unapokuwa kiongozi katika nchi hii, lazima ujitofautishe. Ninamshangaa sana Mheshimiwa Keissy kwa sababu haelewi kitu anachokiongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeenda shule, hivi Hazina accountability yake iko wapi? Si ipo kwenye Wizara ya Fedha? Sasa unaponiambia kwamba hii shilingi bilioni 50 haihusiki katika Wizara hii, naomba niikatae taarifa yake na niendelee na mchango wangu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende moja kwa moja kuchangia suala la Benki ya Wanawake. Nimekwisha kujitambulisha mimi ni Mbunge na mwakilishi wa wanawake Mkoa wa Mwanza na Tanzania nzima. Suala la Benki ya Wanawake tumekuwa tukilipigia kelele sana humu ndani. Nitaendelea kusema nina amini Wizara ya Fedha ndio ambayo inahusika kupitia Hazina. Treasury ndiyo wanahusika kupeleka fedha, walioenda shule wote watakuwa wananielewa.(Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Serikali itusaidie kupeleka fedha katika benki hii ili kuiongezea mtaji ili wanawake waweze kukopa kila sehemu. Matawi yawepo Tanzania nzima ili wanawake waweze kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie dakika zangu mbili kuhusu suala la malipo ya watu ambao walikuwa wanafanya kazi Afrika Mashariki. Ninaamini suala hili la watu ambao walikua wanafanya kazi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki linamgusa kama sio mimi, litakugusa wewe na litamgusa Mbunge mwingine… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kwa maandishi katika Wizara hii. Kwanza nianze na suala la wabunifu wa teknolojia katika nchi hii. Nchi hii wapo watu ambao wana ubunifu wa kutumia teknolojia, lakini hawajulikani wala kutambulika na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa Kampuni ya Young Scientist Tanzania ambayo huwasaidia kuwaendeleza vijana chipukizi wa ubunifu na teknolojia, Kampuni hii mwaka huu imewapa tuzo vijana wawili wa Shule ya Sekondari Morogoro ambao ni Edmund na John Method. Pia vijana hao Kampuni imewapelekea kusoma Dublin University huko Ireland kwa ajili ya kuendeleza vipaji vyao vya ubunifu na ufumbuzi wa teknolojia. Nashauri Serikali iwe inafuatilia vijana wabunifu kama hawa ili wanapomaliza masomo yao, Serikali iwashawishi kurudi nchini ili kutumia ujuzi wao kusaidia maendeleo ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuboresha mishahara ya Walimu pamoja na mazingira ya kufanyia kazi kama vile nyumba, umeme na maji. Hii itaondoa upungufu wa Walimu mashuleni hususan shule za pembezoni mwa Miji. Walimu wengi wanapopelekwa au kupangiwa na Serikali shule za vijijini huwa hawaendi kutokana na mazingira magumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inahitaji kuongeza juhudi katika kutoa elimu bora ili kushindana na nchi nyingine duniani. Nasema hivi kwani wanafunzi wengi humaliza Kidato cha Nne ambayo ni elimu ya awali bila kujua kusoma na kuandika vizuri, lakini pia hata kutokuwa na uwezo na kujieleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kutoa mchango wangu kwa maandishi katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa meli mpya katika Ziwa Victoria, kutafungua fursa za biashara katika Mikoa ya Mwanza na Kagera kwani mazao mengi kutoka mikoa hiyo hutegemea usafiri wa maji. Vile vile meli hiyo itasaidia usafirishaji wa abiria na mizigo. Hivyo niiombe Serikali kutenga fedha katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ununuzi wa meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa upanuzi wa barabara ya Furahisha hadi Pasiansi Airport, hii imesaidia kupunguza foleni na msongamano wa magari. Naiomba Serikali ianze kufanya tathmini ya kuendelea kupunguza msongamano katika Jiji la Mwanza kwa kufungua barabara zitakazoondoa msongamano katikati ya Jiji. Barabara hizo ni za:- Buhongwa
– Rwanhima – Kishiri – Igoma na barabara ya Mkuyuni – Mahina – Nyakato – Buzuruga na barabara ya Butimba – Fisheries – SAUT – Mkolani. Kwa kufungua barabara hizi kutaondoa msongamano katikati ya Jiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya Wizara hii lakini sijaona fedha zilizotengwa kwa ajili ya ununuzi wa kivuko cha base Wilaya ya Ilemela kwenye Jimbo la Mheshimiwa Angelina Mabula ambapo pia Mheshimiwa Rais aliahidi wakati wa kampeni za uchaguzi 2015. Katika vikao vya RCC tulikubaliana kununua kivuko hicho. Niiombe Serikali itenge fedha za kununua kivuko hicho ambacho kitawasaidia wakazi wa kisiwa hicho cha base wapatao 600 na zaidi hususan akinamama ambao wanahitaji kuvuka kuja mjini kwa ajili ya kujifungua hasa wanapopata rufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nashukuru na naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwa maandishi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia vifo vya mama na mtoto katika Mkoa wa Mwanza ambavyo ni asilimia 21 kitaifa. Idadi hii ni kubwa sana. Vifo vya uzazi kwa asilimia 37 hutokana na kutokwa damu nyingi wakati wa kujifungua, hivyo kama mama asipowahishwa hospitali hupoteza maisha, na hii husababishwa na vituo vya afya kuwa mbali. Vilevile asilimia 21 ya vifo vya wajawazito hutokana na kuchelewa kufanya maamuzi ya njia ya kujifungua hususan upasuaji wa kupanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza pia una upungufu wa vituo vya afya vinavyotoa huduma ya upasuaji. Hivyo, tunaiomba Serikali ituongezee vituo vya afya vyenye huduma za upasuaji hususan Wilaya za Ukerewe, Sengerema na Magu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake. Mfuko huu utengewe fedha ili kusaidia Halmashauri kuwakopesha akina mama kwa kujumuisha na asilimia tano ya mapato ya ndani ya Halmashauri. Kwa kufanya hivyo, akina mama watakuwa wamewezeshwa kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kuzipongeza Halmashauri za Mkoa wa Mwanza ambazo zimefanikiwa kutenga na kupeleka fedha kwenye vikundi vya akina mama zikiwemo Halmashauri za Ilemela, Sengerema, Mwanza Jiji, Kwimba, Misungwi na Buchosa. Niiombe Wizara
husika kufuatilia Halmashauri ambazo hazikutoa fedha hizo kama vile Halmashauri za Ukerewe na Magu na kuzitaka Halmashauri hizo kupeleka fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee suala la Benki ya Wanawake. Benki hii ilianzishwa ili kusaidia akina mama kukopesheka kwa riba nafuu, lakini benki hii haitengewi fedha za kutosha kama alivyoahidi Mheshimiwa Waziri Ummy wakati akihutubia kwenye maadhimisho ya sita ya wanawake duniani 2016, kwamba Wizara itatenga shilingi bilioni mbili kila mwaka lakini katika mwaka huu imetengwa shilingi milioni 69 tu. Naiomba Serikali itenge fedha ya kutosha ili benki hii iweze kukopesha kwa riba ndogo ya asilimia 10 mpaka 12 na pia kuongeza matawi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Serikali iangalie suala la CT scan katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando kwani inategemewa na mikoa ya jirani kama Kagera na Mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni mimba za utotoni; hizi pia zinachangia vifo vya mama na mtoto. Niiombe Serikali ilete marekebisho ya Sheria ya Ndoa ili kusaidia watoto wanaoolewa na umri mdogo na hivyo kupelekea mimba za utotoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa utangulizi ufuatao. Sasa tunaelekea mwisho wa miaka mitano ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa 2016 - 2021 na sasa tuko katika Mpango wa Nne ambao ndiyo tuko tunaujadili sasa hivi. Naomba wakati tunajadili Mpango huu wa Nne wa Maendeleo ya Taifa, naomba tuangalie baadhi ya mambo ambayo kama itapendeza Wizara kama walivyoahidi katika kitabu chao kwamba wanachukua maoni yetu kwa sababu haya ni Mapendekezo ya Mpango, kwa hiyo, kama itawapendeza kuchukua mawazo yangu basi nitashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza kwa kuangalia hali ya uchumi katika Taifa hili la Tanzania. Hali ya uchumi katika Taifa hili la Tanzania kutokana na taarifa ya Mheshimiwa Waziri, anasema kwamba hali ya uchumi imeimarika. Hata hivyo, ukiangalia hali ya uchumi wa mwananchi mmoja mmoja bado ni duni, purchasing na buying power ya wananchi imepungua na iko chini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwananchi wa hali ya kawaida kwa sasa hivi, kwanza kabisa vifaa vya ujenzi vimepanda bei kiasi kwamba mwananchi tu wa kawaida hata kujenga nyumba inamuwia vigumu. Ukiangalia katika zile basic needs, nyumba ni kitu cha msingi sana lakini maisha ya mwananchi bado yako duni kiasi kwamba hawezi kuwa na uwezo wa kujenga nyumba kwa sababu vifaa vya ujenzi vimepanda bei. Hata katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri ameeleza kwamba mfumuko wa bei kwa sasa hivi umepungua. Ni kweli katika vitu vidogo vidogo kama vile vyakula lakini masuala yale ya msingi ambayo yanaweza kusaidia mwananchi kuwa na maendeleo hali bado sio nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia vilevile wakati uchumi wa Taifa wenyewe unakua lakini uchumi wa wananchi unaendelea kuwa duni, bado wapo wezi, mimi nawaita wezi. Kumezuka janga kwa hawa watu wenye hizi betting centers, nitazitaja, sasa hivi kuna Tatu Mzuka, Premier Bet, Moja Bet na Biko, hawa wote ni wezi ambao wanaiba fedha za wananchi katika mifuko yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema hawa ni wezi kwa sababu hiki wanachokifanya ni sawasawa na upatu. Sisi wenyewe wananchi ndiyo tunatoa pesa zetu halafu baadaye wanatokea wanatangaza kwamba kuna mshindi ameshinda shilingi milioni 100. Hata hivyo, ukiangalia wananchi ndiyo wame-contribute zile fedha, zimefika shilingi bilioni moja huyu mtu amekusanya, kwa kuwa yeye hana mtaji, halafu mwisho wa siku sasa, wananchi kwenye mifuko yao wanabaki bila fedha, halafu anatokea mtu mmoja anatangazwa mshindi anachukua shilingi milioni 100 yeye katajirika. Huu ni wizi wa waziwazi kabisa, mimi nimeangalia nimeona hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba kuishauri Serikali kwamba sasa tunapojadili Mpango huu wa Nne hebu tuangalie tunasaidiaje wananchi kutoka katika hali ya umaskini ili waweze kujikomboa na kuwa na maisha mazuri. Kwa sababu hauwezi ukajinadi ukasema kwamba uchumi wa nchi unakua wakati hali ya wananchi wako inazidi kuwa duni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali kama ikipendeza wachukue maoni haya, waweke mkakati wa kuhakikisha wanazi-control hizi betting centers, waangalie ni kwa namna gani hizi betting centers...

T A A R I F A . . .

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimu sana mdogo wangu Mheshimiwa Salome na naamini kabisa ame-scrutinize kitu ambacho amekisema kabla hajanipa taarifa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, japokuwa hawa watu wa betting centers wapo kisheria lakini mimi naangalia ni namna gani wanaiba fedha katika mifuko ya wananchi. Ndiyo maana naendelea kuishauri Serikali iangalie ni namna gani wanaweza kuzi-control hizi betting centers ili wasiendelee kuchukua fedha katika mifuko ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimeshaishauri Serikali iangalie controlling ya hizo betting centers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kutokana na hali ya wananchi wetu kuendelea kuwa duni, solution mojawapo ambayo Serikali inaweza kuifanya ni kuongeza Government expenditure. Serikali ijitahidi katika kuhakikisha kwamba inatumia sana ili kule chini mzunguko wa fedha uendelee kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ambapo sasa tunaenda katika Mpango huu wa Nne, ukiangalia fedha za maendeleo katika Halmashauri zetu haziendi. Waheshimiwa Wabunge wataniunga mkono kwa sababu wamekuwa wakisema mara kwa mara humu ndani kwamba fedha za maendeleo katika Halmashauri zetu haziendi, ni sifuri kabisa. Sasa unategemea ni kwa namna gani hawa wananchi wanaweza wakawa na maendeleo wakati fedha za maendeleo kwenye Halmashauri haziendi, ina maana kule kwenye Halmashauri zetu hakuna miradi yoyote ambayo inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ukiangalia katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri katika changamoto ambazo amezisema, amesema changamoto mojawapo ni kutokuweza kuwalipa wakandarasi wa ndani pamoja na wazabuni mbalimbali. Nashauri Serikali basi iweze kuweka mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba wakandarasi na hawa wazabuni wanalipwa kwa wakati ili wananchi waweze kuwa na mzunguko wa fedha waweze kujikimu kimaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nionglee suala la deni la Taifa. Mara kwa mara nimekuwa nikiongelea suala la deni la Taifa na leo sitaweza kuliongelea kwa muda mrefu kwa sababu ya muda kutoniruhusu. Deni la Taifa tunaliona linaendelea kuongezeka. Kwa taarifa ambazo siyo rasmi, deni letu la Taifa sasa limeongezeka kwa asilimia 46.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sipingani kwamba tusikope, tukope lakini lazima tuweke mikakati madhubuti ya kuhakikisha kwamba tunaweka control ya ukomo wa deni. Tusiwe tunakaa tunasema kwamba deni letu ni stahimilivu na hivyo tuendelee tu kukopa pasipokuwa na mpango mkakati wa ukomo wa kukopa, tutakopa mpaka shilingi ngapi na tunavyozikopa hizo fedha tutazikopa kwa sababu ya nini? Ningefurahi sana tunapotengeneza Mpango huu wa Nne tuangalie ni kwa namna gani tunali-control deni letu la Taifa ili lisiendelee kuwa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sasa hivi karibia asilimia 35 ya mapato ya ndani inatumika kulipa deni la Taifa. Hii inasababisha baadhi ya miradi kuzorota na kutoweza kukamilika kwa wakati. Kwa hiyo, nashauri Serikali iangalie namna gani ya kuweza kuli-control deni hili la Taifa ili tusije tukajikuta tunaingia katika nchi ambazo na zenyewe zimeingia katika debt stress, zimepata stress ya madeni. Ukiangalia nchi kama Mozambique wamekuwa wakikopa na kukopa, Serikali inakuwa inasema kwamba deni ni stahimilivu hatimaye sasa hivi Mozambique imeletewa kuwa ni nchi ambayo imeingia katika debt stress. Sitapenda Serikali ya Tanzania au nchi ya Tanzania iingie katika kuwa na debt stress. Kwa hiyo, nashauri Serikali iweke good management ya deni letu la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kama muda wangu unaruhusu, naomba Serikali iweke mkakati wa kuwakikisha kwamba wanaachana na suala la kukopa mikopo ambayo ina riba kubwa, wakope mikopo yenye riba nafuu ili tuweze kuwa na uwezo wa services deni letu. Kwa maana kwamba tukifanya hivyo, basi tunaweza kuchochea maendeleo ya wananchi katika nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine naomba kushauri Serikali ijitahidi kuwawezesha wataalam kupata mafunzo ya negotiation skills ili wanapoenda kujadili mikataba ya kukopa haya madeni ya Taifa waangalie zile contract ambazo wanaweka kwamba zina manufaa gani katika nchi yetu. Sasa hivi China amekuwa anakopesha nchi za Afrika na China ni mjanja sana anamkopesha mpaka Mmarekani lakini anapokuja kuzikopesha nchi za Afrika anajuwa sisi hatuna negotiation skills, kwa hiyo, yeye analeta masharti yake na sisi tunayakubali wakati yale masharti yanakuwa siyo mazuri. Unakuta Mchina anakukopesha halafu anakwambia wafanyakazi wake ndiyo wafanye kazi wakati sisi wananchi wetu wapo na wana uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti naiomba Serikali iweze kuangalia wanapokwenda kujadili mikataba ya kimataifa kuhusu mikopo wajue wanakopa kwa ajili gani, kwa sababu gani na mikopo ya bei nafuu. Nashukuru sana naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, pia naomba nimshukuru sana Mungu kwa kuendelea kunipa afya njema ili niendele kutoa michango yangu katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nitoe salamu za pongezi kwa Serikali. Naomba kuanza kwa kuipongeza Serikali kwa namna ambavyo wameweza kuleta upanuzi wa uwanja wa ndege wa Mwanza, tumeuona watu wote tumekuwa tukisafiri na tunaona uwanja wa ndege wa Mwanza kwa hali ambayo ulikuwa nayo lakini Serikali imewekeza pesa pale na kuweza kufanya upanuzi wa uwanja ule wa ndege wa Mwanza.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Seriakli kwa sababu imeweza kuwalipa fidia wananchi ambao walikuwa wana migogoro na Jeshi katika maeneo ya Lukobe na maeneo mengine ambayo walikuwa na migogoro katika Mkoa wa Mwanza. Tunaipongeza sana Serikali kwa sababu tumekuwa tukiiomba sana kuwalipa fidia wananchi hawa ambao wamekuwa wakiingia kwenye migogoro na Jeshi. Pia naomba kuiomba Serikali waendelee kutusaidia kuwalipa fidia wananchi ambao wapo katika uwanja wa ndege ambao unapanuliwa. Wawalipe fidia wananchi hawa ili kuweza kuepusha migogoro inayoendelea katika upanuzi ule wa uwanja wa ndege na kutufanya, kama wananchi wa Mkoa wa Mwanza au Wabunge wa Mkoa wa Mwanza kupunguza kura zetu. Ninaamini kwamba Serikali ni sikivu na itaweza kulisikia hilo na kulifanyiakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa salamu hizo za pongezi, naomba sasa kuendelea kuipongeza Serikali kuhusiana na suala la hoja iliyoko mbele yetu ya Bajeti Kuu ya Serikali. Bajeti hii kama hatutatoa pongezi kwa Serikali kwa namna ambavyo imejitahdii kuhakikisha kwamba inazifanyia kazi changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa mara kadhaa katika Bunge hili na Wabunge wa Bunge hili tutakuwa hatujaitendea haki Serikali. Wanasema ‘mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni’ name sina budi kuipongeza Serikali kwa sababu bajeti hii ambayo iko mbele yetu tunaijadili siku hii ya leo imezitatua changamoto mbalimbali za kodi lakini pamoja na tozo mbalimbali ambazo zimekuwa ni kero pamoja na yote wameendelea kuhakikisha kwamba wanaweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara wote walio wakubwa, wa kati pamoja na wafanyabiashara wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siipongezi tu hivi mtu anaweza akadhani ninapongeza pasipokuwa na evidence. Ukiangalia Serikali imeweza kufanya marekebisho ya ulipaji wa kodi mbalimbali. Wamepunguza ulipaji wa kodi kutoka kiwango cha shilingi 150,000 hadi shilingi 100,000 lakini pia wamepunguza malipo ya kodi kutoa 318,000 hadi 135,000. Waheshimiwa Wabunge mkiangalia ukurasa wa 41 hadi ukurasa wa 42 mtaona ni namna gani Serikali imeweza kuingatia ushauri ambao umekuwa ukitolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, siishii hapo; katika miaka mitatu mfululizo ndani ya Bunge hili nimekuwa nikiishauri Serikali mara kwa mara kuhakikisha kwamba wale wafanyabiashara ambao wanaanza biashara zao wasitozwe kodi kabla hawajaanza biashara. Kwa nini nisiipongeze Serikali kama imeweza kuyachukua maoni yale na kuweza kuyafanyiakazi kwa kufanya marekebisho ya Sheria na kuhakikisha wkamba inatoa tax holiday kwa wale wafanyabiashara ndani ya miezi sita kama unaanza biashara yako unapewa unafuu wa kutokulipa kodi hadi baada ya miezi sita ina maana kwamba baada ya miezi sita ukiwa kama mfanya biashara unaweza kuwa umekwishakufahamu kuwa biashara yako ina mtiririko gani, unapata faida ama unapata hasara, pamoja na hapo utaweza kukadiriwa kodi vizuri na hiyo itasababisha wafanyabiashara wengi kulipa kodi kwa hiari bila kukwepa kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuipongeza bajeti hii ya Serikali, tumekuwa na changamoto mbalimbali pia ambazo zinatokea. Bajeti hii ina changamoto kubwa moja ambayo inawagusa Wanawake wa Tanzania. Nikiwa kama Mbunge ambae nawakilisha Wanawake wa Tanzania nitakuwa sijawatendea haki wale ambao ninawawakilisha hawana uwezo wa kuja kuyasema haya ndani ya Bunge hili bali wametuma wawakilishi wao, kama sitawasema nitakuwa sijawatendea haki.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imeonesha kutokuwa na gender responsive, kwa sababu gani nasema hivyo? Kuna suala la Serikali ukiangalia pale katika ukurasa wa 34 wamefuta msamaha wa kodi la ongezeko la thamani katika taulo za kike. Suala la kufuta msamaha huu kwa kweli kama Wanawake wawakilishi ndani ya Bunge hili hatujalielewa suala hili, ni kwa nini Serikali imekuja na wazo hili, walikaa wakafikiria nini. Ukiangalia suala la taulo hizi za kike hazitumiwi tu na watoto au wanafunzi ambao wako mashuleni bali zinatumiwa na asilimia kubwa sana ya Watanzania ambao ni wanawake. Wanatumia watoto wa kike, wanatumia akinamama ambao wametoka kujifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kujifungua mwanamama anahitaji kutumia taulo za kike ndani ya siku 14 au zaidi kwa hiyo Serikali ilipokuwa imetoa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani katika taulo hizi za kike walitarajia na walikuwa wana nia njema na tuliwapongeza kwamba walikuwa wana nia njema ya kuhakikisha kwamba kunakuwa kuna unafuu wa gharama katika kununua taulo hizi za kile lakini kwa bahari mbaya sana suala ambalo Serikali na wananchi tulilitarajia halikutokea lakini Serikali imekuja na kusema kwamba wanaondoa tena ule msamaha wa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Mbunge nimekuwa nikijiuliza, Serikali ina mkono mrefu. Wajibu mmojawapo wa Serikali ni kuhakikisha kwamba wana- regulate bei ya bidhaa zinapokuwa zipo sokoni. Kama Serikali inaweza leo hii sukari ikapanda bei Serikali ikatia mkono wake, ikatoa kauli yake, kutoa bei elekezi ya sukari ili kila mwananchi aweze ku-afford kununua sukari, vipi kuhusiana na taulo za kike suala ambalo linawagusa wananchi karibu asilimia 50 ambao ni wanawake?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali baada ya kuwa wametoa ule msamaha, wameshindwa vipi kuhakikisha kwamba wana-monitor suala la ongezeko au punguzo la bei? Serikali imeshindwa vipi kukaa na wafanyabiashara hawa kuwaambia kwamba tumetoa msamaha wa kodi tunaomba mpunguze bei na kuwapa bei elekezi kuwa kiasi kadhaa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi taulo hizi za kike zinanunuliwa kwa gharama ya Sh.2000 hadi Sh.3500, hiyo ni gharama kubwa sana. Kwa Mtanzania tu wa hali ya kawaida hawezi kununua taulo hizi za kike. Ndiyo maana tukaitaka Serikali kutusaidia na ndiyo maana na wenyewe wakatoa msamaha huo wa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali irudi tena mezani iangalie suala hili linawezekana kwa sababu limekuwa likiwezekana kwenye bidhaa zingine kama vile petroli, sukari, Serikali imekuwa ikiweka mkono wake, kwa nini Serikali isitusaidie sisi wanawake? Mnataka mpaka wanawake wote wa Bunge hili tugome pamoja na wanaume naamini watanisaidia kwa sababu wao ndiyo wanunuzi wa taulo hizi za kike. Hatuzinunui sisi wenyewe, akina baba hawa ndiyo wanaozinunua hizo taulo za kike. Ina maana mwanaume kama yupo ndani ya nyumba ana mke wake ambaye ndio mama, watoto wa kike watano, ndugu, jamaa na marafiki anaishi nao mule ndani ya nyumba ambao ni wanawake, mwanaume si ndiye anayenunua? Kwa hiyo, leo nikisema wanawake tuanzishe mgomo kwa ajili ya suala hili, naamini wanaume watatuunga mkono na tutaweza kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatutaki kufika huko kwa sababu tunaamini kwamba Serikali hii ni sikivu. Kama imekuwa ikiyasikia maoni mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge na kuyatafakari na kuyafanyia kazi, naamini hata hili haliwashindi wanaweza wakalitafakari na wakalifanyia kazi. Huo ndiyo ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutoa ushauri huo, pia naomba niishauri Serikali kwamba vipo viwanda vyetu, kwa mfano kuna Kiwanda cha cha MSD, Mkoa wa Pwani, pia kuna kiwanda kingine cha madawa Mkoani Simiyu, naishauri Serikali ivielekeze viwanda hivi kuanzisha production line ya hizi taulo za kike. Hiyo itasaidia taulo hizi kupatikana ndani ya nchi na hivyo kuleta unafuu wa bei na wananchi wanaweza wakazifikia kwa urahisi zaidi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na namshukuru Mungu kwa kuendelea kunipa uwezo wa kushiriki katika Bunge hili Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kumpongeza mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu, mama ambaye ameufahamu wajibu wake kwa nafasi aliyopewa kwa kuwaangalia wanawake wa Tanzania kwamba wana upungufu wa damu na hivyo kuweza kuhamasisha katika Mkoa wa Dodoma na watu wamekwenda kujitolea damu. Tunaamini kwamba mama yetu Mama Samia Suluhu ataendelea kutambua na mikoa mingine kwamba wanawake wengi wanakufa kila siku kwa ajili ya upungufu wa damu pale wanapokwenda kujifungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa pongezi hizo, sasa naomba nijikite katika kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Afya. Natokea Mkoa wa Mwanza ambapo tuna Wilaya ya Ilemela ambayo bado ni changa ilianzishwa mwaka 2012. Kwa masikitiko makubwa sana Wilaya ya Ilemela hakuna Hospitali ya Wilaya. Kwa bahati mbaya sana Halmashauri ya Ilemela wakati imekatwa kutoka kwenye Halmashauri ya Jiji la Nyamagana iliomba shilingi milioni 300. Baada ya kupatiwa fedha hizo Halmashauri hii imeweza kutumia shilingi milioni 193 kuanzisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana kwa kuanza na jengo la emergence. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilipokuwa nikitazama kwenye vitabu mbalimbali vya bajeti ya Wizara ya Afya sijaona ni wapi ambapo Serikali imetenga pesa kwa ajili ya kuweza kutusaidia Wilaya ya Ilemela kujenga majengo yetu ya Hospitali ya Wilaya ya Ilemela. Hivyo basi, namuomba Waziri wa Afya, dada yangu pale, aweze kutusaidia kiasi ambacho kimeombwa na Halmashauri ya Ilemela shilingi bilioni mbili na milioni mia tatu kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Ilemela. Nitamuomba Waziri wetu wa Afya anaporudi kujibu hoja basi atusaidie kutueleza ametenga kiasi gani au Serikali imetenga kiasi gani kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naongelea suala la upungufu wa dawa. Tumeona katika Mkoa wa Mwanza limefunguliwa duka la MSD, lakini kwa masikitiko makubwa sana dawa katika lile duka hakuna. Namuomba Waziri aweze kufanya uchunguzi kwamba katika hilo duka ni dawa gani zimepelekwa au hizi dawa zimeishia wapi. Yawezekana dawa zimepelekwa lakini zimebaki zina-hang somewhere na hazijaweza kufika katika hili duka la MSD ambalo limefunguliwa pale katika Hospitali ya Rufaa ya Sekou-Toure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana, Mkoa wa Mwanza hakuna mashine za CT-Scan. Watu wengi wamekuwa wakifa kutokana na matatizo ya ubongo. Tunafahamu kabisa CT-Scan ina uwezo wa kutambua mgonjwa ana matatizo gani kwenye kichwa ili kuweza kuepuka mgonjwa kupata stroke. Tumeweza kuwa na wagonjwa wengi sana ambao wanapata stroke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Waziri atakapokuja aje na majibu sahihi tena ya uhakika kwamba katika Mkoa wa Mwanza hususani Hospitali ya Bugando ambayo imesemekana kwamba kuna CT-Scan lakini ninao uhakika wa asilimia mia moja, hata sasa hivi Waziri akisema tupande ndege twende Mwanza au twende kwa basi au kwa gari gani lakini twende Mwanza sasa hivi tukakague Hospitali ya Bugando CT-Scan hakuna. Naomba sana Wizara yetu iweze kuwa makini katika kuangalia vifaa ambavyo vinakuwa vinapelekwa je vimefika au havijafika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukazia kuomba CT-Scan katika Hospitali yetu ya Rufaa ya Sekou-Toure. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Ummy aliahidi na kusema kwamba CT-Scan itapelekwa mara moja iwezekanavyo. Hivyo basi, nakuomba Waziri wakati ukiangalia bajeti yako utusaidie pale Mwanza utupelekee CT-Scan katika Hospitali yetu ya Rufaa pale Mwanza ya Sekou- Toure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza inazo kata 19. Mheshimiwa Rais alitoa ari kwamba kuwepo na vituo vya afya katika kila kata, lakini pawepo na zahanati katika kila kijiji. Kwa masikitiko makubwa sana Wilaya ya Ilemela tunazo kata kumi na tisa lakini tuna vituo vya afya vitatu kikiwepo Kituo cha Sangabuye, Bugogwa pamoja na Karume. Kwa bahati mbaya hivi vituo vyote vitatu havina hadhi ya kuitwa vituo vya afya. Ukiangalia katika Kituo cha Karume hakina huduma nzuri, vitanda hakuna, kuna vitanda viwili tu, hakuna kitanda cha akina mama kujifungulia, huduma ya kufanyiwa upasuaji akina mama pia hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Ummy kwa kuwa na wewe ni mwanamama na unafahamu kabisa kina mama tunapopata matatizo wakati wa kujifungua, utusaidie. Kwa kuwa umesema akina mama wengi wanapoteza maisha wakati wakipata haki yao ya msingi ya kutuletea watoto hapa duniani, naomba utusaidie basi kutuboreshea vituo vya afya hivi vichache tu ambavyo vipo katika Wilaya ya Ilemela. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini namuomba pia Waziri aweze kuisaidia Halmashauri ya Ilemela kwani ni change, kila inapotenga pesa kwa ajili ya kusaidia kutoa huduma bora za afya haiwezi kufanikiwa kwa sababu inakuwa ina majukumu mengi na hivyo kuielemea halmashauri. Hivyo, namuomba Waziri aweze kutusaidia basi Wilaya ya Ilemela tuondokane na hivi vituo vitatu basi walau atuongezee vituo viwili ili tuweze kusogeza huduma karibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia leo nilikuwa sina mengi sana lakini naongelea pia kuhusiana na suala zima la Benki ya Wanawake. Naomba Serikali iweze kuiangalia hii Benki ya Wanawake. Mheshimiwa Mbunge ambaye amechangia katika hili suala la huduma ya Benki ya Wanawake amesema kwamba Serikali imetenga shilingi milioni 900, ninasita mimi katika kusoma bajeti ya Serikali, nimeona Serikali imetenga shilingi milioni 500 tu na siyo shilingi milioni 900. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri Ummy aliwahi kusema kwamba atatoa shilingi bilioni mbili kila mwaka. Kwa mwaka huu wa fedha kama Serikali imetenga shilingi milioni 500 tu sioni kama tutafikia malengo ya kuweza kuiendeleza Benki hii ya Wanawake hapa Tanzania. Ukiangalia benki hii sasa hivi ina mtaji wa shilingi bilioni 20 tu peke yake. Kwa hiyo, kama katika mwaka huu watafanikiwa kuongeza hizo shilingi milioni 500 ambazo zimetengwa bado benki hii haiwezi kuwasaidia wanawake. Hakuna matawi mengi hapa nchini, kuna matawi machache sana ambayo yako kwenye mikoa michache nadhani ni mitano au nane...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini pia, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuipongeza Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na hasahasa kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri, Mheshimiwa Lukuvi pamoja na Mheshimiwa Mama yangu Mama Angelina. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea suala zima la National Housing, kama walivyochangia Wabunge wengi kuhusiana na suala la National Housing kujenga nyumba ambazo zinaonekana ni nyumba za bei nafuu kwa kinadharia tu, lakini nyumba hizi si kwa ajili ya wale wananchi wasiojiweza kwa sababu, nyumba hizi za National Housing ni nyumba ambazo ni za gharama sana. Kwa mfano, katika Hotuba yake Mheshimiwa Waziri page number 58 mpaka page number 61 ameonesha kwamba nyumba za National Housing zinajengwa ili kuweza kuwasaidia wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia hapa mfano Mkoa wa Mwanza, Wilaya ya Ilemela tunazo nyumba za National Housing ambazo zimejengwa Buswelu. Nyumba hizi zilikuwa ni nyumba nzuri, lakini sasa zinauzwa bei ya juu, zinauzwa kwa gharama ya shilingi milioni 80, sasa najiuliza je, mwananchi wa hali ya kawaida, hali ya chini, anao uwezo wa kununua nyumba ya shilingi milioni 80?
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapomwambia kwamba, aende kuchukua mkopo benki, tunafahamu wote kwamba, unapoenda kuchukua mkopo benki unaulipa kwa riba. Hivi kweli, je, tunaposema hii nyumba inauzwa milioni 80 mwananchi huyu aende kuchukua mkopo benki unakuwa umemsaidia mwananchi wa hali ya chini au unakuwa sasa umezidi kumgandamiza. Hii ni kwa sababu, anapokwenda kuchukua mkopo benki riba itakuwa ni kubwa; akikopa milioni 80 anaweza akarudisha milioni 120 kwa hesabu za harakaharaka kwa sababu, mimi pia ni mtaalam wa masuala ya benki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi naishauri Serikali iweze kusaidia shirika hili. Kwa mfano, shirika hili ukiangalia mara nyingi wanasema kwamba, nyumba hizi zinakuwa ni za gharama kwa sababu ya kupitisha miundombinu kwa sababu halmashauri zinakuwa zimewapa eneo lakini miundombinu kama vile maji, umeme, barabara, inakuwa haipo. Kwa hiyo, nashauri kwamba, basi Serikali au Wizara husika isaidie kupitisha miundombinu ya barabara, maji pamoja na umeme, ili pale shirika hili linapoanza kujenga hizo nyumba basi ziwe za bei rahisi, ili kuweza kuwakwamua wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia, niweze kuishauri Serikali kwamba, Shirika la National Housing liweze kujenga nyumba za bei nafuu kwenye makazi ya vijijini kwa sababu, vijijini ndiko sehemu ambako tuseme asilimia kubwa ya wananchi hapa nchini Tanzania wanaishi, lakini makazi yao bado ni duni sana. Kwa hiyo, naishauri Serikali kupitia Shirika lake hili la National Housing kujenga makazi ya bei nafuu huko vijijini.
Mheshimiwa Mweyekiti, lakini pia, ukiangalia sehemu nyingi za vijijini tayari kunakuwa kuna makazi yamekwishajengwa pale, kulikoni Serikali iende kujenga sehemu nyingine, naishauri Serikali kwamba, itumie lile eneo la kijiji husika kubomoa zile nyumba zilizopo kwa kuwapa elimu wananchi kwamba, ni kwa nini nyumba zinabomolewa, lakini kuweza kunyanyua majengo aidha ya magorofa au majengo ya kawaida, ili wananchi wa eneo hilo waweze kufaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia maeneo mengi ya watu wanaoishi vijijini ni wakulima. Kwa hiyo, watakapokuwa wamejenga nyumba zile wananchi wanaweza wakapangishwa au wakauziwa kwa bei nafuu na wakulima hawa wakaweza kulipa kidogo kidogo hatimaye kumaliza deni na nyumba kuwa za kwao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la squatters, squatter imekuwa ni suala ambalo ni sugu sana hapa nchini Tanzania. Naishauri Serikali kwamba, izisaidie fedha Halmashauri, ili ziweze kusaidia kurasimisha makazi na hii inaweza ikasaidia Serikali pia kupata mapato kwa sababu, katika hizi squatter hawa wananchi wanalipa tu mapato kwa Halmashauri lakini Serikali inakosa mapato kwa kupitia property tax. Kwa hiyo, nashauri Serikali iweze kuzisaidia halmashauri hususan Mkoa wa Mwanza, Wilaya ya Ilemela, watusaidie fedha kwa ajili ya kurasimisha makazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia wakazi wa Mkoa wa Mwanza wanaishi sana kwenye milima, matokeo yake tunaona disaster zinatokea, wananchi wanaangukiwa na mawe. Kwa hiyo, utaona kama maeneo yale yakiweza kupimwa na Serikali na kuweza kurasimishwa kwa wananchi kihalali, basi tutakuwa tumeondokana na hizo disaster za wananchi kuangukiwa na mawe pia hata kuondoa hili suala zima la bomoabomoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikijiuliza, kuna tatizo moja limetokea hapo Mkoani Mwanza, Wilaya ya Ilemela, kuna rada imejengwa katika Mlima wa Kiseke, rada ile imesababisha makazi 500 sasa yatakwenda kubomolewa ili kupisha rada hiyo ya Mlima huo wa Kiseke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza, hivi wakati hawa wananchi wanaanza kujenga kuanzia nyumba ya kwanza mpaka zimefika nyumba 500 na sasa zinahitajika kubomolewa, Serikali ilikuwa wapi? Haikuwaona hawa wananchi toka wanaanza kujenga nyumba moja mpaka zinafika nyumba 500? Leo hii waseme kwamba, wanataka kuzibomoa nyumba hizo, ili wananchi hawa wapishe eneo hilo la rada, kwa sababu, kwa kweli ni eneo ambalo limekuwa ni hatarishi! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri sana Serikali, wananchi wanapovamia sehemu moja kwenda kujenga, basi mwananchi wa kwanza anapoanza kujenga ile nyumba moja, Serikali iweze kutoa elimu kwa wale wananchi, ili wasiendelee kuathirika pale nyumba zinapokuwa nyingi na hatimaye kubomolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, mtakapokuja kuhitimisha hoja hii mnisaidie tu kunipa majibu kwamba, je Wananchi wale wa Kiseke wategemee nini? Je, watalipwa fidia? Kama watalipwa fidia, ni vigezo gani vitatumika kuangalia katika kulipa fidia hizo? Hilo naomba sana mnisaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kuongelea suala zima la hizi mashine ambazo zilitolewa na Shirika la National Housing, mashine za kufyatulia matofali kwa vijana wetu. Ukiangalia mashine hizi za kufyatulia matofali kwa kweli zina malengo mazuri tu; kwanza ni kupata ajira kwa vijana, lakini pili, kujenga nyumba ambazo ni za bei nafuu na pia ni imara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia vijana hawa wameshindwa kupata soko la kuuza haya matofali ambayo wamepatiwa hizo mashine na hatimaye hata kuna mikoa ambayo iliathirika na wakanyanganywa hizo mashine kwa mfano Mkoa wa Katavi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini je, Serikali kwa nini inashindwa kuwasaidia hawa vijana ili wanapokuwa wanafatua yale matofali basi wapate tenda hususani kwenye halmashauri zetu, wapate tenda za kujenga. Lakini unakuta kwamba kwenye halmashauri wanatoa tenda kwa watu wengine na wanatumia matofali haya ya kufyatua ya kawaida. Hivi hawa vijana ambao mmewapa hizi mashine kwa nini Serikali isiwasaidie ili na wao waweze kujiendeleza? Pia na hizi Halmashauri nazisihi kwamba ziendelee kutoa mitaji kwa hawa vijana ambao wamegawiwa hizo mashine za kufyatua matofali ili waweze kusaidia kufyatua matofali mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo sikuwa na mengi, ni hayo tu, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na pia namshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye anaendelea kunijaalia afya njema ili na mimi niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu hasa katika Wizara hii ya Fedha na Mipango. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba niipongeze Wizara ya Fedha kwa sababu imekuja na mpango ambao wananchi sasa wanaanza kuwa na imani kwamba kama mpango huu utatekelezwa basi wananchi wote wataenda kufaidika na nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika michango yangu. Kwanza kabisa naomba kuchangia suala zima la Deni la Taifa. Ukiangalia Deni la Taifa, faida zake kubwa sana ni katika kusaidia kuchangia katika maendeleo ya Taifa hususan katika kuendeleza miundombinu kama vile barabara, viwanja vya ndege, reli na hata kwenye afya pia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kusikitisha sana ni kwamba Deni la Taifa limekuwa likiongezeka mwaka hadi mwaka. Kwa mfano, ninazo data kidogo hapa; mwaka 2005 hadi mwaka 2010 Deni la Taifa lilikuwa yapata trilioni 10; mwaka 2010 hadi mwaka 2012 Deni la Taifa liliongezeka hadi kufikia trilioni 14, lakini mwaka 2015 hadi sasa Deni la Taifa sasa limefikia trilioni 41; hii inasikitisha sana. Kwa sababu gani nasema inasikitisha? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Deni la Taifa linaongezeka lakini wananchi bado hali inazidi kuwa ni ngumu. Swali langu sasa kwa Waziri, na naomba Waziri atakapokuja anisaidie walau kunipa majibu lakini si mimi peke yangu wala Bunge lako hili Tukufu bali hata wananchi wote wanaonisikiliza sasa hivi, kwamba; ni kwa sababu gani deni hili lime-shoot kutoka trilioni 14 mwaka 2012 hadi kufikia trilioni 41 kwa mwaka 2015. Ninaomba Waziri atakapokuja basi aje na ufafanuzi utakaoweza kuwasaidia wananchi wa Tanzania kuelewa ni kwa nini deni hili linazidi kuongezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia na Wabunge wenzangu deni hili linapokuwa linazidi kuongezeka ni kwamba kila Mtanzania katika nchi yetu anazidi kuwa na ongezeko la kulipa deni hili. Kwa mahesabu, bahati mbaya hesabu nilipata “F” kwa hiyo, sijui namna ya kupiga deni hili kwa kila Mtanzania lakini mtanisaidia pamoja na Waziri, kwamba hivi deni hili ni lini basi litaweza kuwafaidisha wananchi wa Tanzania. Deni linaongezeka, barabara bado ni mbovu, kila Mbunge akisimama hapa wakati wa kipindi cha maswali na majibu hata wakati wa maswali ya nyongeza utasikia kila mtu analalamika kuhusiana na suala zima la barabara lakini hata hivyo, masuala ya maji, kila Mbunge anasimama hapa akiwakilisha wananchi wake kwa kulalamikia suala la maji. Hivi kwa nini Deni la Taifa linazidi kuongezeka? Ninaomba na ninamtaka Waziri atakapokuja anieleze tu ni kwa nini Deni la Tafa linazidi kuongezeka na wakati wananchi bado wana maisha ya chini au la sivyo naomba nitoe taarifa kabisa kwamba nitashika shilingi ya Mheshimiwa Waziri itakapofika muda wake, kama hatakuja na majibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Nampongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu amesaidia. Tunaona kabisa ongezeko la mapato hapa nchini sasa limeongezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna changamoto ambazo zipo. Kwa mfano, baada ya kuongezeka kwa mapato haya, Halmashauri zetu hazifaidiki na ongezeko la Pato la Taifa. Nasema hivyo kwa sababu kwenye Halmashauri zetu kuna kero mbalimbali ambazo zimefutwa ambazo zimekuwa zikiwakera wananchi, na hata Mheshimiwa Rais nae pia amekuwa akiziongelea kero hizi. Baada ya kero hizi kufutwa hakuna mbadala wa mapato ambao umekuwepo katika Halmashauri zetu na ndiyo maana unakuta kwamba hata Halmashauri inapotenga fedha kwa ajili ya kuondoa changamoto za barabara, maji hata afya, hawawezi kufikia malengo yao kwa sababu ongezeko la pato katika Halmashauri zetu – mapato yanapokuwa yanakusanywa malengo ya Halmashauri yanakuwa ni makubwa kiasi cha kwamba Halmashauri zinashindwa hata ku-prioritize kwamba tuanze na lipi na tumalizie na lipi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi ninaishauri Serikali walau katika Wizara hii kwa sababu Wizara hii ndiyo Wizara ambayo inakusanya mapato ya Taifa kwa ukubwa kabisa. Wizara hii naweza nikaisema kama ni Wizara nono, Wizara ambayo imeshiba, basi tunaomba kwamba Wizara ya Fedha iweze kupeleka fedha ziwafikie wananchi hasa katika Halmashauri zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano mdogo tu; katika Halmashuri zetu tuna mpango mzuri sana ambao tumeuweka wakuzitenga asilimia10 ambayo asilimia tano inatakiwa kwenda kwa wanawake na asilimia tano iende kwa vijana. Lakini ukiangalia Halmashauri nyingi kwa tathmini ya haraka haraka zimekuwa hazitengi fedha hizi na si kwa sababu wanafanya makusudi kutokutenga fedha hizi iliziweze kuwafikia wananchi, lakini ni kwa sababu ya kulemewa na mzigo wa mipango ambayo wanakuwa nayo kiasi cha kwamba ile fedha hata kama inakuwa imetengwa matokeo yake inakuja kufanya dharura.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano; nikiongelea katika Jimbo la Ilemela ambalo ni Jimbo la Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ardhi Mama Angelina Mabula, kule tumekuwa na mipango mizuri sana, kila mwaka wamekuwa wakitenga fedha hizi lakini inapofika wakati kwamba sasa fedha hizi ziweze kugawiwa kwa wananchi hasa wanawake na vijana unakuta fedha hizi zinatumika katika kutengeneza barabara. Ukiangalia katika Wilaya ya Ilemela, ni Wilaya ambayo bado Halmashauri yetu ni changa. Ninaitaka na ninaiomba Serikali kwa unyenyekevu mkubwa sana kwamba iweze kuangalia Halmashauri zetu ili basi waweze kuongezewa fedha walau ziweze kuwasaidia wanawake hususan akina mama kama vile mama lishe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mzunguko wa fedha umekuwa ukionekana kama unaishia huku juu tu, yaani unaishia kwenye sehemu za juu, yaani wananchi wa hali ya juu ndiyo ambao wanafaidika na pesa. Sasa unapoongelea Pato la Taifa limeongezeka wakati mwananchi wa chini bado fedha haijamfikia ni masikitiko makubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ninamuomba Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake anisaidie tu kuja na mikakati kwamba Serikali imejiwekea mikakati gani ya kuziba mianya ya fedha ambazo imekuwa ikipoteza, kwa sababu inawezekana tukakusanya pesa nyingi lakini wako watu ambao kazi yao wamekaa kuchungulia hizi pesa na kuweza kujinufaisha wao wenyewe matokeo yake wananchi hawafaidiki na fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niongelee suala la shilingi milioni 50 kila kijiji. Tulipokuwa tukizunguka katika kampeni zetu za mwaka huu. Kila mwananchi anakuuliza kuhusiana na suala la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji. Swali kwa Waziri ni kwamba, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba kila mwananchi ananufaika na pesa. Ukiangalia kwa mfano katika ukurasa wa 24 Maoni ya Kamati au Uchambuzi wa Kamati, unaonesha kwamba Tanzania tunavyo vijiji 19,600, tunahitaji shilingi bilioni 980. Serikali imetenga asilimia sita tu ambayo ni shilingi bilioni 59 na milioni 500. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata nisipoendeea kusoma taarifa hii ya Kamati lakini utaona kabisa kwamba tunayo changamoto ambayo bado ni kubwa sana kwa sababu inaonesha wazi sasa ni vijiji vichache sana, yapata vijiji 1,000 ndiyo ambavyo vitafaidika na hii shilingi milioni 50. Ni masikitiko makubwa sana. Hivi tunaenda kurudi vipi kule kwa wananchi? Tutawaeleza nini wananchi wetu kuhusiana na suala la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji? Naiomba Serikali ifuate ushauri ambao umetolewa na Kamati ya Bajeti kwamba waongeze pesa walau ifikie asilimia 20 japokuwa na fedha hii bado ni ndogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema kwamba Sheria ya Manunuzi iletwe…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii ili pia niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu. Pia naendelea kumshukuru Mungu kwa sababu ameendelea kunipigania na kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoanza kuchangia Mpango huu wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2017/2018 nitapenda sana niwapitishe katika kitabu hiki kwa kutumia pages. Kwanza kabisa, naomba tuangalie ukurasa wa pili wa Mpango huu wa Maendeleo ya Taifa, kifungu cha 1.4 kinazungumzia utaratibu wa kuandaa Mapendekezo ya Mpango. Katika utaratibu wa kuandaa Mapendekezo ya Mpango umeangalia mambo mbalimbali ikiwemo hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa wakati anafungua Bunge la Kumi na Moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Rais anafungua Bunge hili la Kumi na Moja wote tulimsikiliza kwa makini. Mheshimiwa Rais aliongea vizuri sana na hotuba yake ilikuwa inalenga katika kuwakomboa wananchi wa Tanzania. Mheshimiwa Rais aliongea mambo mengi sana na moja ya jambo ambalo alisisitiza ni viwanda. Mheshimiwa Rais alisisitiza kwamba anataka Tanzania iwe ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimepitia mpango huu vizuri sana, ukiangalia viwanda vimeongelewa kwa kuguswaguswa, nasikitika sana kusema hilo. Kwa maana kwamba mpango haujajikita katika kusema waziwazi kwamba ni viwanda gani ambavyo sasa vinaenda kuangaliwa na mpango huu. Hivyo basi, napata wasiwasi kama kweli sisi tuko tayari kufuata ushauri ambao Mheshimiwa Rais alikuwa akiuongea? Aliongea katika kampeni zake, aliongea katika kulifungua Bunge hili na mpaka sasa bado Mheshimiwa Rais anaendelea kuongea na kusisitiza kuhusiana na suala zima la viwanda, napata wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, kwamba anapotuletea mpango mwezi Mei nadhani baada ya kuchukua mapendekezo yetu Waheshimiwa Wabunge, namsihi sana katika mpango wake atuelezee ni viwanda gani hasa ambavyo anaenda kuviweka katika mpango wake. Vivyo hivyo atakapokuja kutenga bajeti atenge bajeti ambayo kweli ita-reflect kwamba sasa Tanzania inaenda kuwa Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la maji. Hatutaweza kuwa na viwanda nchini Tanzania na hatutaweza kamwe kufikia malengo ya Mheshimiwa Rais ambayo ni malengo mazuri sana kama haitakuwa Tanzania ambayo wananchi wa kawaida, mwananchi aliyeko kijijini anaweza akapata maji wakati wowote atakapoyahitaji. Nasema hivi kwa sababu gani? Maji ni kiungo kikubwa sana kwani yanaweza yakasaidia katika kilimo. Ukiangalia sasa hivi naweza nikasema nchi hii inaelekea kwenye jangwa kwa sababu hakuna maji kabisa. Nchi imekuwa na ukame na hata watu wa Idara ya Hali ya Hewa pia wametabiri kwamba sasa hivi hakutakuwa na mvua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Mwanza kuna kilimo cha pamba na mazao mengine mbalimbali lakini wananchi wanashindwa kulima kwa sababu ya ukosefu wa maji. Hata hivyo, ukiangalia katika mpango huu, kama ninavyosema na nitarudia kusema maji yanatajwa tu kwamba maji, maji yanafanya nini? Tuna mikakati gani kwamba maji sasa yanaenda kupatikana Tanzania? Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Mipango atakapoleta mpango atuletee mpango mkakati kwamba anaenda kufanya nini ili kuhakikisha kwamba Tanzania inaenda kuwa na maji? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kuna suala pia la irrigation scheme, nimeliona limetajwa humu katika mpango lakini halioneshi dhamira kwamba kweli tunataka kufanya irrigation scheme hapa nchini Tanzania ili kuwezesha kilimo ambacho ndicho kitakachotupeleka kwenye viwanda. Kwa sababu tutakapoanzisha viwanda tunatarajia kuwa na raw materials, tunaenda kupata wapi hizi raw materials kama hatutaweza kuimarisha kilimo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tena niongelee suala kubwa sana ambalo Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, ameliongelea wakati wa kampeni zake. Wakati wa kampeni zake akifanya ufunguzi pale Jangwani aliongea kwa ari kubwa sana na alikuwa anamaanisha. Najua anamaanisha kwa sababu niliona jinsi alivyoongea. Hakuna mtu aliyemtuma kuongea, alijituma mwenyewe kwa sababu anao uchungu na anayo nia ya kuwasaidia Watanzania ili waondokane na umaskini. Mheshimiwa Rais alisema kwamba atahakikisha Serikali yake inatoa milioni 50 katika kila kijiji, hii ni katika kuwawezesha Watanzania kuondokana na umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunapitisha bajeti hapa niliongea kwa uchungu sana kuhusiana na suala la milioni 50. Nashukuru kwamba Serikali ilisikiliza na ikaongeza pesa kidogo hadi kufikia kutenga bajeti ya shilingi bilioni 49. Hata hivyo wakati nikichangia katika bajeti iliyopita nilisema kwamba shilingi bilioni 49 ambazo zimetengwa bado hazitoshi. Tuna vijiji 13,000 hizi hela ambazo zimetengwa bado ni ndogo sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, natambua juhudi za Serikali, natambua juhudi ambazo Mheshimiwa Waziri wa Fedha anazifanya kuhusiana na suala la kutimiza ahadi ya Rais ya milioni 50, ili kuweza kuwakomboa Watanzania kutokana na umaskini, namwomba na ninamsihi sana katika mpango wake ajaribu kuelezea ni vijiji vingapi ambavyo vitaweza kupata hii shilingi milioni 50. Atuoneshe na atuelezee wazi kwa sababu tunapata kigugumizi tunapozunguka kwenye Majimbo yetu, wananchi wameandaa vikundi mbalimbali wamevi-register, wako kamili wanasubiri milioni 50 ya Mheshimiwa Rais, lakini sasa kama hatutataja kwenye mpango wananchi tutawaambia nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha atakapoleta mpango uwe umejumuisha ni vijiji vingapi, vitapata shilingi ngapi, ni mkoa gani kwa Tanzania nzima? Hivyo vijiji avitaje ili tuweze kufahamu kwamba sasa mimi Mkoa wangu wa Mwanza vijiji kadhaa vitapata na Mkoa wa Tanga vijiji kadhaa vitapata. Naomba sana kuishauri Serikali kuhusu hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea suala la afya. Juzi nilisimama hapa kwa uchungu mkubwa sana na nikasema kuhusiana na suala la dawa. Kumekuwa na upungufu wa dawa na hata Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu alikiri kuwepo kwa upungufu wa dawa. Tumekuwa tukiilaumu Wizara ya Afya ambapo sasa hivi naomba kabisa niombe radhi kwa Wizara ya Afya kwa sababu naamini kabisa nimewakosea kuwaonea nilitakiwa nimlaumu Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa sababu yeye ndiye ambaye anahusika na suala zima la kutenga fedha kwa ajili ya dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wa Mipango atakapoleta Mpango katika Bunge hili, atuoneshe wazi kwamba sasa ni fedha kiasi gani au ni mikakati gani aliyonayo ya kuhakikisha dawa zinapatikana Tanzania nzima ili akinamama wasiteseke. Akinamama ambao wanateseka ni wajawazito wanakwenda kwenye hospitali wanaishia kupimwa ujauzito tu basi, kuangalia vipimo kwamba mimba imefikia katika hatua gani lakini dawa hakuna! Inapotokea anapata tatizo lolote mama huyu anaandikiwa dawa anaambiwa nenda kanunue kwenye pharmacy, pesa hana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunayo nia ya kuwasaidia Watanzania namsihi sana…
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu nadhani bado upo, dakika 15?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ameweza kunijalia afya njema ili niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianze kuongelea suala zima la uwezeshaji wananchi kiuchumi. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukurasa wa 15 ameongelea suala la uwezeshaji wanawake kiuchumi na ukisoma pale ndani ameandika kuhusiana na maendeleo ya wanawake kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake wa mwaka 2007 ambao unalenga kuwawezesha wanawake kiuchumi ili waweze kukopesheka. Lakini kwenye bajeti ya mwaka 2016/2017 Mfuko huu wa Maendeleo ya Wanawake haukutengewa fedha zozote. Naomba niiombe Serikali itusaidie kutenga fedha kwa ajili ya kuuwezesha huu Mfuko
wa Maendeleo ya Wanawake ili wanawake waweze kukopesheka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikuwa nina kikao na wanawake wa Mkoa wa Mwanza, kwa kweli swali zito ambalo nilikumbana nalo ni huu Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake. Wanauliza Mfuko huu wa Maendeleo ya Wanawake unawasaidiaje wanawake ili waweze kujishughulisha na masuala mazima ya uchumi? Ukiangalia wanawake wengi wa Mkoa wa Mwanza wanajishughulisha na shughuli mbalimbali kama vile mama lishe hata wamachinga pia wapo ambao ni wanawake lakini kama Mfuko huu wa Wanawake usipotengewa fedha, ni jinsi gani
wanawake wataweza kujikwamua kiuchumi? Hivyo, naomba sana katika bajeti ya Waziri Mkuu basi suala hili la wanawake liweze kuangaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika mataifa makubwa duniani na hata yale ya nchi jirani kama vile Zimbabwe, Malawi na Msumbiji na nchi nyingine hata Kenya tu hapo jirani, wamekuwa wakiliangalia suala zima la wanawake katika kutenga bajeti. Ukiangalia hapa Tanzania katika bajeti zote ambazo zimekuwa zikitengwa suala la mwanamke limekuwa liki-lag behind. Unakuta mwanamke anatajwa katika maeneo machache sana. Sisi wanawake tumeamua sasa kuiambia Serikali, lakini kuiomba kwa unyenyekevu mkubwa sana kwamba sasa ianze kuangalia suala zima linalowahusu wanawake. Kwa sababu wanawake ndiyo ambao wanachangia katika pato la Taifa na hivyo basi naomba wasiachwe nyuma. Hivyo basi, naendelea kuisihi Serikali yangu kuuangalia mfuko huu na kuweza kutenga fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Wizara hii ya Afya inayoshughulika na wanawake, huyu mama ambaye ndiyo ameshikilia hii Wizara, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, tunapomuweka kuwa yeye ndiyo mshika dhamana ya wanawake hapa Tanzania halafu mfuko ule haujatengewa fedha, ina maana tunamdhoofisha huyu dada katika kuisimamia hii Wizara ya wanawake. Kwa hiyo, naendelea kusisitiza na kuiomba Serikali, kwa mwaka huu wa fedha iweze kutoa fedha na kuweka kwenye mfuko ule ili kuweza kuwasaidia wanawake kwenye VICOBA ambavyo wamevianzisha waweze kujikopesha na kuweza kujikwamua kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niongelee suala la afya. Katika hotuba ya Waziri Mkuu ukiangalia ameongelea suala zima la afya na amesisitiza kwa kusema kwamba Serikali inaendelea kujenga vituo vya afya ili kuhakikisha wanawake nchini wanapata huduma za kiafya
vizuri. Ukiangalia katika afya kuna pillars tatu, yaani zahanati, vituo vya afya pamoja na hospitali za Wilaya. Kule ndiko ambako zile basic needs za afya zinaanzia. Katika Mkoa wa Mwanza tunavyo vituo vya afya vya Serikali 46 tu ukiunganisha na vituo vingine vya binafsi jumla ni vituo 388.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hivi vituo 46 va Serikali ni vituo vinne tu katika mkoa wa Mwanza ndivyo ambavyo vinatoa huduma ya upasuaji. Wanawake wengi wamekuwa wakipoteza maisha wakati wa kuleta watoto hapa duniani. Ukiangalia idadi ya vifo vya akina mama Mkoa wa Mwanza ni 21% na hiyo inatokana na kukosa huduma za upasuaji katika vituo vyetu vya afya. Hivyo basi, naiomba Serikali iweze kutusaidia katika Mkoa wa Mwanza kuwezesha kutupa vituo vya afya ambavyo vinaweza vikatoa huduma za afya ili viweze kuongezeka kutoka vituo vinne tufikie hata vituo 15 kwa kuanzia ili wanawake wasiweze kuendelea kupoteza maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Sustainable Development Goals, goal mojawapo ni
kuhakikisha huduma za mama na mtoto na za wajawazito zinapatikana kwa urahisi na kuendelea kuondoa vile vifo vya mama na mtoto. Kwa hiyo, kama tumeingia mkataba huu
wa kwenye Sustaibale Development Goals, naiomba Serikali iweze kutusaidia katika Mkoa wa Mwanza kutuboreshea vituo vyetu vya afya ili viweze kutoa huduma ya upasuaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka siku moja hapa nilipokuwa nikiuliza swali langu la nyongeza niliuliza suala la wanawake wanavyopata huduma za upasuaji lakini hawapati huduma za upasuaji kwa kupangiwa. Nilipokuwa naongea kile kitu nafahamu kwa sababu mama anapopata ujauzito kuna matatizo ambayo huwa yanaonekana kwenyescan kabla hata muda wake wa kujifungua haujafika. Kwa hiyo, kama tatizo limeshaonekana na kwenye kituo cha afya kuna huduma ya upasuaji, mama huyu anatakiwa apangiwe ni lini na siku gani atakayofanyiwa upasuaji ili kuweza kuokoa maisha yake yeye kama mama lakini pia na maisha ya mtoto yule ambaye anamleta duniani. Kina mama wengi sana wamekuwa wakipoteza maisha yao lakini mtoto anabaki kwa sababu ya kutoa damu nyingi na matatizo mengine
mbalimbali ambayo yanawakumba akina mama wakati wa kujifungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika hotuba ya Waziri Mkuu wameeleza ni namna gani bajeti ya vifaa tiba pamoja na dawa imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 hadi shilingi bilioni 251. Katika kuongezeka kule sisi Mkoa wa Mwanza naiomba tu Serikali katika bajeti hii ya mwaka huu iweze kutusaidia CT Scan, Mkoa wa Mwanza hatuna CT Scan. Ukiangalia CT Scan inasaidia katika mambo mengi sana si tu wanawake. Kuna watoto wanazaliwa kule na vichwa vikubwa Mkoa wa Mwanza lakini na Kanda ya Ziwa kwa ujumla… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Mnamo tarehe 5 Mei, 2016 nilisimama katika Bunge lako Tukufu kuwatetea watoto ambao wanaolewa wakiwa na umri chini ya mika 15. Nami naomba niahidi kwamba nitaendelea na ari hii hii ya kuwatetea watoto wa kike ambao wamekuwa wakipoteza ndoto zao wakiolewa katika umri mdogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na utangulizi huo, Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inaonekana ni sheria ambayo inambagua mtoto wa kike ambapo katika kifungu kile cha 13 na 17, kinamtaka mtoto wa kike kuolewa akiwa na umri wa miaka 15 wakati mtoto wa kiume anaoa akiwa na umri wa miaka 18. Ukiangalia katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 13 nitanukuu, inasema:-
“(1) Watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ya ubaguzi wowote kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria”.
(2) Ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka yoyote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuweka sharti lolote ambalo lina ubaguzi wa dhahiri au kwa taathira yake.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sheria hii ya Ndoa ya mwaka 1971 utaona ni kwa namna gani inakinzana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumbagua mtoto wa kike ambaye anatakiwa kuolewa na umri wa miaka 15 ilihali mtoto wa kiume anatakiwa kuoa akiwa na umri wa miaka 18 na kuendelea. Ni jukumu letu sasa sisi kama wanawake na wawakilishi wa watoto wa kike na wanawake wote Tanzania nzima lakini tukishirikiana na Waheshimiwa Wabunge wote bila kujali rika na kujali jinsia kuwatetea watoto wa kike ili na wao pia waweze kutimiza ndoto zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona madhara ya ndoa yakiwemo ya kiafya. Watoto wengi wa kike wanapokuwa wanaolewa na umri mdogo wa miaka 15, kiafya watoto hawa wanakuwa hawajapevuka katika maumbile yao na hivyo basi kitu hiki kinasababisha watoto hawa wanapopata ujauzito, hizo tunaziita ni mimba za utotoni kwa sababu zile ni mimba ambazo bado yule mtoto hajapevuka maumbile yake na madhara makubwa ambayo yanatokea ni vifo vya akinamama. Naamini kabisa Serikali haitapenda kuona vifo vya wanawake vikiendelea kutokea ambavyo vinasababishwa na sheria hii ya ndoa za utotoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia madhara mengine ya ndoa za utotoni ni vifo vya watoto wachanga ambao wanazaliwa na akinamama ambao bado hawajapevuka. Kitu kingine, wasichana wanakosa elimu na kuna msemo unaosema kwamba unapompa elimu mtoto wa kike umesaidia jamii nzima, hili linaonekana wazi kabisa. Wapo Waheshimiwa sasa hivi humu ndani wakiamua watoe shuhuda zao kwa kweli kila mtu atastaajabu. Basi ni jukumu letu sisi Waheshimiwa Wabunge kuiomba au kuishawishi Serikali iweze kutusaidia kurekebisha Sheria hii ya Ndoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na madhara ambayo yanawakuta wasichana, kwa sababu wasichana ndiyo waathirika wakubwa, wanapoolewa na umri mdogo, kwa nini tunasema Sheria ya Ndoa ibadilishwe. Mchakato wa kuomba Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ifanyiwe
marekebisho haukuanza leo. Hivyo naamini kwamba Bunge hili halitakuwa la kwanza kuishawishi Serikali kuleta mabadiliko ya Sheria ya Ndoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato huu ulianza mwaka 1984 ambapo Umoja wa Wanawake Tanzania waliishauri Serikali kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria kwamba Serikali irekebishe Sheria hii ya Ndoa kwa sababu walizunguka Tanzania nzima na wakaona kwamba watoto wengi wa kike wanapata hasara kubwa sana wanapoolewa na umri mdogo. Kwa hiyo, utaona kwamba mchakato huu haukuanza leo ulianza siku nyingi sana mwaka 1984 wakati sheria imeundwa mwaka 1971, mchakato huu ulianza mapema sana. Wanawake Tanzania waliona ni kwa namna gani watoto wa kike wanaathirika katika kuolewa na umri mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato huu pia mwaka 1994 Tume ya Mabadiliko ya Sheria baada ya kupokea maoni mbalimbali kutoka kwenye NGO’s mbalimbali walileta pia mapendekezo yao. Kama ningepata nafasi ya kukuletea hapo mezani na wewe pia ukayapitia mapendekezo ya Tume hii ambayo ilishauri kwamba Serikali ifanyie marekebisho Sheria hii ya Ndoa. Pamoja na changamoto zote ambazo zinaonekana za kimila na za dini lakini bado Tume hii ilishauri Serikali kufanyia marekebisho Sheria hiyo ya Ndoa ili kuwanusuru watoto wa kike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tumeingia mikataba mbalimbali ya kimataifa ukiwepo Mkataba wa Haki za Watoto, Mkataba wa Kutokomeza Aina Zozote zile za Ubaguzi hapa Nchini Tanzania na kwingineko. Pia Sustainable Development Goals inazingatia sana kutokomeza ndoa za utotoni ifikapo mwaka 2030. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, juzi juzi tu hapa ilitoka hukumu dada mmoja anayeitwa Rabeca Gyumi alipeleka mapendekezo yake Mahakamani kuhusiana na kubadilishwa kwa Sheria hii ya Ndoa. Kama tunavyofahamu Mahakama ndiyo sehemu pekee ambayo wanaweza
kutusaidia kutafsiri sheria na hapa ninayo nakala ya hukumu. Katika hukumu hii iliyotolewa na Mahakama inapendekeza Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kubadilisha Sheria hii ya Ndoa kile kifungu cha 13 na 17 ambacho kinapendekeza umri wa mtoto wa kike kuolewa kuwa miaka 15 na wa kiume kuoa akiwa na miaka 18. Kwa hiyo, hukumu imetoka ikieleza au ikiitaka Serikali kubadilisha vifungu hivyo vya Sheria ya Ndoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo sina mengi sana ya kuongea lakini naomba nihitimishe kwa kusema kwamba, sisi Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tukikaa kimya bila kuwasemea watoto wa kike kwa kweli watu wengi huko nje watabaki wanatushangaa. Nasema hivi kwa sababu nimekuwa nikifuatilia sana kwenye TV, wanawake wanalia na kutoa machozi tena wanabaki wanauliza, wako wapi wanawake wa Tanzania waweze kututetea watoto wetu wasiolewe katika umri mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ndoa hizi wanaoathirika sana ni watoto wetu wa kike. Japokuwa kuna juhudi za Serikali ambazo kwa kweli zimeonekana na siwezi kukataa kwamba juhudi za Serikali hazijaonekana. Tunaona marekebisho ya Sheria ya Elimu ya mwaka 2016 ambayo inataka watoto wasiolewe chini ya umri wa miaka 15 au wakiwa wako shuleni. Hata hivyo, ukiangalia sheria hii inawabagua wale ambao wapo nje ya mfumo wa elimu. Kwa hiyo, ni ombi langu kwa Serikali kutusaidia tu kutekeleza hii hukumu ambayo imekwisha kutoka au la sivyo naomba wanapokuja kuhitimisha hoja yao…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichangie kuhusiana na suala zima la COSOTA. COSOTA ni kitengo ambacho kilianzishwa makusudi kabisa kwa ajili ya kuwasaidia wasanii ili waweze kumiliki kazi zao ipasavyo, lakini pia kuondokana na wizi ambao unafanywa na watu kutokana na hizi kazi za wasanii. Cha kustaajabisha ni kwamba kitengo hichi cha COSOTA kimepelekwa katika Wizara ya Viwanda na Biashara. Niishauri Serikali kwamba kitengo hiki cha COSOTA kiondoke kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara na kuweza kurudi katika Wizara hii ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu ukiangalia COSOTA kazi yao ni kuwatetea wasanii, kulinda kazi zao na hizo hati miliki zao. Sasa unapokipeleka kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara yenyewe inajihusisha na mambo mengine kabisa. Sasa unapopeleka chombo hiki kwenye Wizara kama ile tusitegemee accountability ya chombo hiki. Nashauri Serikali iweze kurudisha chombo hiki cha COSOTA kwenye Wizara ya Habari na Utamaduni kwa ajili ya accountability yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia chombo hiki ni muhimu sana katika kulinda haki za wasanii. Tunaona kazi za wasanii zinaibiwa sana, lakini adhabu yake pia inayotolewa kutokana na ile sheria ambayo tulipitisha hapa Bungeni ya hati miliki yaani copy right kwa kweli ni ndogo sana. Unakuta sheria inasema kwamba kazi za msanii zinapokuwa zimeibiwa mtu aliyeiba zile kazi anaadhibiwa kwa adhabu ya faini ya shilingi milioni tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni juzi tu hapa tuliona mtu ameiba kontena kubwa sana la kazi za wasanii na adhabu aliyopewa ni faini ya shilingi milioni tano. Hivi mimi nikiiba kazi ya msanii ambayo najua kabisa kwamba kazi hii inaenda kunipa pesa zaidi hata zaidi ya shilingi milioni 20 halafu leo unaniambia kwamba nilipe faini ya shilingi milioni tano, sitaacha kweli kuwaibiwa wasanii kazi zao? Hili liko wazi kabisa, kazi za wasanii zitaendelea kuibiwa endapo tutaacha COSOTA kutosimamia kazi hizi za wasanii na adhabu zake kuwa ni ndogo kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri nini Serikali? Naishauri Serikali adhabu za kuiba kazi za wasanii ziwe sawa kabisa na adhabu za unyang’anyi, sijui kama niko sahihi lakini nazungumzia piracy. Kwenye Penal Code mtu akiwa amefanya unyang’anyi (piracy) anapelekwa jela kwa muda wa miaka saba, lakini sasa kazi za wasanii zinapoibiwa tunaona kama ni kitu cha kawaida tu. Nashauri kabisa Serikali iweze kuuchukulia huu wizi wa kazi za wasanii kuwa kama wizi mwingine tu wa aina ya piracy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni wasanii ambapo wanakuwa wanaibiwa kazi zao kwa namna ya kupigwa kwa mfano redioni. Let’s say mwanamuziki ambapo nyimbo zake zinakuwa zinapigwa redioni, lakini huyu mwanamuziki hafaidiki na wimbo wake kupigwa redioni. Nitakupa mfano mzuri sana. Tuna wanamuziki maarufu sana hapa Tanzania nikimtaja King Kiki kila mtu anawaza kitambaa cheupe na ndani ya Bunge hili naamini kabisa hata leo hii nikisema mimi natoa offer kwa Waheshimiwa Wabunge kwenda kumsikiliza King Kiki wote mtakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukumbuke na kuweka kichwani kwamba tunapomsikiliza huyu mwanamuziki King Kiki pamoja na kupiga wimbo wake wa kitambaa cheupe, tunashangilia kwenye sherehe kwenye harusi au popote pale ambapo mtu unakuwa na shughuli yako nzuri, unamaliza kushangilia pale lakini huyu mwanamuziki King Kiki ukienda kumuangalia na ile kazi ambayo wewe umekuwa ukiishangilia anafaidika vipi? Unamchukua huyu mwanamuziki unamuweka hapa haendani kabisa na muziki ambao unapigwa redioni na kushangiliwa na kila Mtanzania. Naomba sana Serikali iweze kusimamia na kuzilinda kazi za wasanii ili waweze kufaidika ili basi siku moja hawa wasanii tuwaone kwamba kweli wanaendana na muziki ambao sisi Watanzania tunapenda kuusikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusiana na suala la kurekebisha Sheria ya Hati Miliki. Nasema hivi kwa sababu gani? Sheria hii kwanza imeshapendekezwa katika kamati mbalimbali kwamba iweze kufanyiwa marekebisho. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo ambao tuna- deal na hizi kanuni ambazo zinatungwa. Tuliipitia hii Sheria ya Hati Miliki tukaona upungufu uliomo katika sheria hiyo. Upungufu mmoja ambao tuliugundua ni kwamba wakati sheria hii inatungwa hakukuwepo na ushirikishwaji wa wadau ambao ni wasanii, wanamichezo na wadau wengine mbalimbali ambao wanahusika katika suala zima la utamaduni na sanaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo linakuja kwamba pale ambapo wale wadau ambao wanahusika na sheria inayotungwa hawajashirikishwa, utaona kabisa kunakuwa na gap ambalo limewekwa. Kwa hiyo, naomba sana pamoja na mambo mengine yote ambayo yanaitaka sheria hii kurekebishwa kama vile adhabu, kwa sababu katika sheria hii ndiyo pale tunaona ile adhabu ya kuwaadhibu wale ambao wameiba kazi za wasanii ndiyo hiyo ya shilingi milioni tano ambayo ni ndogo.

Kwa hiyo, kama ungeshirikisha wale wadau ambao wanahusika ungeona wangeweza kupendekeza jambo ambalo mimi leo nalisema na kulipendekeza mbele ya Serikali kwamba iwe ni adhabu sawa kabisa na wizi mwingine. Kwa hiyo, nashauri kabisa Serikali iweze kutuletea hii sheria ili tuweze kuifanyia marekebisho lakini baada ya kuwa imewashirikisha wadau wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti jambo la mwisho ni suala la michezo. Suala la michezo hapa Tanzania hatulichukulii maanani kabisa. Ukiangalia enzi za zamani michezo ilikuwa ni kitu ambacho tunakitilia maanani sana. Kila mahali unakoenda hata mwanafunzi anafahamu kabisa kwamba mimi bila kushiriki michezo sitaweza kufaulu darasani kwa sababu darasani tulikuwa tunaambiwa hivyo na walimu wetu kwamba ili uweze kufanya vizuri lazima ushiriki michezo. Hiyo inaendana kabisa na usemi kwamba ili mtu uwe active kwenye akili zako lazima kwanza ushiriki michezo kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, suala la michezo hapa Tanzania tumekuwa tukilichukulia tu kama jambo la kawaida. Mimi naiomba Serikali ianze sasa kurudisha michezo mashuleni na kuweza kuweka mkazo huko mashuleni ili hawa akina Samatta watokee kule na hata kina Diamond hawa watokee kule kule kwa sababu hata kwenye kuhamasisha michezo kuna uimbaji pia huko mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika kurahisisha suala hili ili liweze kufanyika vizuri ni kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba tuanzishe sports academy. Nchi kama Kenya tu msifikiri kwamba Kenya wanaposhinda kwenye Olympics mkadhani kwamba huwa wanaenda tu, wanaibuana from no where wanapelekwa kwenye michezo, hapana! Kenya wanachukua wachezaji kutoka kwenye sports academy zao na sasa hivi Kenya wanaenda mbali zaidi wanaleta International Sports Academy ambayo hiyo sasa itakuwa inawarahisishia kuweza kutoa wachezaji kutoka kwenye zile sports academy kuwapeleka kwenda kufanya mashindano lakini sisi hapa tunaibuana tu, mtu akisema anajua kuogelea anabebwa, anapelekwa, akifika kule ameshindwa. Tanzania hakuna mchezo ambao tumewahi kufanya vizuri hata siku moja. Nadhani hizo ni historia za nyuma kabisa labda hata nilikuwa sijazaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya mapendekezo hayo, naamini Serikali itachukua mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge wote na kuweza kuboresha Sekta hii ya Habari, Utamaduni na Michezo. Nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia katika hotuba ya Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Utalii Tanzania bado inalo jukumu la kuutangaza utalii ndani na nje ya Tanzania. Katika ukurasa wa 100 - 107 katika hotuba ya Waziri imeeleza kwa kirefu namna ambavyo bodi imefanya kazi kuutangaza utalii wa Tanzania ndani na nje kupitia matamasha makubwa yaliyofanyika ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza ni Jiji ambalo limepewa jina la Rock City, hii ni kutokana na mkoa huo kuwa na vivutio vingi vya mawe na majabali yanayoufanya mji huo kupendeza na kuvutia kijiografia. Bismarck Rock ni jiwe kubwa linalopatikana ndani ya maji ya Ziwa Victoria, jiwe hili lilipewa jina la Counselor maarufu wa Ujerumani. Kivutio kingine ni mawe yenye maumbile tofauti tofauti yaliyobebana yanayopatikana katika Milima ya Miama, Wilayani Ilemela, Mkoani Mwanza. Huko pia kuna beach nzuri zilizotulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kivutio kingine ni mawe yanayocheza yanayopatikana katika Kisiwa cha Ukara, Wilaya ya Ukerewe. Mawe hayo yanavutia kwa kuwa hucheza mara yanapoimbiwa nyimbo za kimila na wazee wa kimila. Kivutio kingine ni Nyumba ya Makumbusho ya Bujora. Nyumba hii inaonesha maonesho ya mila na desturi za kabila kubwa Mkoani Mwanza ambalo ni Wasukuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivutio vingine ni Saanane Island na Kirejeshi Game Reserve ambapo wanyama mbalimbali kama vile swala, chui, twiga na simba huonekana kwa urahisi. Serengeti National Park pia inapatikana kwa umbali wa saa mbili tu kutoka Uwanja wa Ndege wa Mwanza, hivyo, kuwa rahisi kufika. Kivutio kingine ni Mnara wa MV Bukoba ambapo watu hutembelea na kutoa heshima zao kwa victims waliozama na kupoteza maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mwanza katikati ya mji kuna mti uliotumiwa na Wakoloni wa Kijerumani kuwanyongea wahalifu. Hivyo basi, niishauri Serikali kupitia Bodi ya Utalii Tanzania kwa kushirikiana na television zote nchini pamoja na majarida ya mashirika ya ndege hapa nchini kutangaza Mji wa Mwanza kama mji wa kitalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote, naunga mkono hoja ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa muda ni mchache nitakuwa na mambo machache sana ya kuchangia siku ya leo, lakini namshukuru Mungu kwa kuweza kunipa afya njema ili niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu, naomba nianze kwa kuchangia suala la uwezeshaji wananchi kiuchumi. Katika ukurasa wa 14 wa hotuba ya Waziri Mkuu ameelezea ni namna gani Serikali imejitahidi kutoa mikopo ile ya asilimia 10 ya Halmashauri kwa akinamama, vijana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mambo machache sana ya kuongelea juu ya suala hii la hii asilimia 10 ambayo inatolewa katika Halmashauri. Halmashauri nyingi sana hapa nchini hazitoi hii asilimia 10 kwa akinamama, vijana pamoja pamoja na watu wenye ulemavu ipasavyo. Hata hivyo, hatujaona Serikali ikichukua hatua yoyote juu ya Halmashauri zile ambazo hazitoi vizuri au hazitengi hii asilimia 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika ukurasa wa 14 wa hotuba ya Waziri Mkuu ameeleza pale kwamba, Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake ulitoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 3.4 kwa vikundi 5,169 katika Halmashauri
153. Swali la kujiuliza hapa katika taarifa hii, tuna Halmashauri takribani 183, Halmashauri ambazo zimetoa mikopo ni 153, je, hizo Halmashauri zingine ambazo hazijatoa mkopo zimechukuliwa hatua gani mpaka kufikia leo hii? Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge hili wamekuwa wakizungumza sana kwamba Halmashauri ambazo hazitoi mikopo zipewe adhabu au kuchukuliwa hatua za kinidhamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wakati tunajadili bajeti tuliona Halmashauri ya Ukerewe pamoja na Halmashauri ya Magu katika Mkoa wa Mwanza, kwa masikitiko makubwa sana Halmashauri hizo hazikutenga kabisa fedha, lakini hatujaona hatua yoyote ile ikichukuliwa. Kwa maana hiyo watu hawa wamekuwa wakiona kwamba hizo pesa wana hiari ya kutoa au kutokutoa na inaonekana kwamba ni sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa stahili hii hatuwezi kuona maendeleo yakiwepo katika Mkoa wa Mwanza. Ukiangalia wanawake wa Mkoa wa Mwanza wanajitahidi sana kujishughulisha na shughuli mbalimbali na wanatarajia kabisa kwamba Halmashauri ziweze kuwasaidia kuwapa hii pesa ya mkopo ili waweze kufanya shughuli zao ndogo ndogo, lakini sasa Wakurugenzi wamekuwa wakifanya sijui niseme ni ukaidi au vipi mpaka hawatoi pesa hizo. Hivyo, naitaka Serikali iweze kuwachukua hatua Wakurugenzi wote ambao hawatengi pesa hizi za asilimia kumi kwa vijana, wanawake pamoja na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, naomba nitoe ushauri mdogo. Fedha hizi ambazo zimekuwa zikitolewa zinatolewa kidogo. Unakuta Halmashauri let’s say inatoa shilingi milioni 200 kwa vikundi vingi, unakuta mwisho wa siku vikundi vinapewa shilingi laki mbili mbili, mwisho wa siku hii pesa ambayo wanapewa inakuwa haileti tija katika kuleta maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoshauri ni jambo moja. Kwa kuwa sasa hivi Serikali ya Awamu ya Tano imekuja na sera ya viwanda basi tuiunge mkono kwamba hizi pesa badala ya hawa akinamama kupewa cash in hand wakakopeshwa na mwisho wake wanashindwa kuzilipa waweze kupatiwa kwa style ya kwamba wanapewa labda mashine kwa ajili ya kuweza kutumia kutengeneza vitu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Mkoa wangu wa Mwanza akinamama wengi wanajishughulisha na suala la kusindika bidhaa mbalimbali ambazo zinatumika majumbani kama vile viungo vya pilau, karanga, nyanya, tomato paste na pineapple ambayo inakuja kuwa pineapple sauce. Kwa hiyo, kuna vitu vingi sana ambavyo wanajishughulisha navyo. Kwa maana hiyo naomba Serikali iwasaidie akinamama hawa badala ya kuwapa pesa basi waweze kuwasaidia mashine ambazo zinaweza zikasaidia kuweza kuleta tija katika utengenezaji wa bidhaa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala zuri ambalo linaweza likafanyika. Katika Mkoa wa Mwanza akinamama nimebahatika kukaa nao kikao na wanahitaji wao vifungashio ili waweze kufungasha hizi bidhaa ndogo ndogo ambazo wanatengeneza. Kwa hiyo, naishauri Serikali Tanzania nzima na Halmashauri zote, fedha hizi badala ya kuwapatia cash kwa mkopo wawasaidie kwamba hawa akinamama …

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba hii, ukurasa wa 23, imeonesha kuwa tayari Mheshimiwa Rais amekwishasaini Sheria ya Kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo ilitungwa na Bunge. Kufuatia kusainiwa kwa sheria hiyo inatakiwa ianze kutumika ili kuhakikisha wadau wa mifuko hiyo wanapata stahiki zao hasa pale wanapoacha kazi kwa kustaafu au kwa kuachishwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, concern kubwa ya wadau ni formula ya kikokotoo kitakachotumika kwa ajili ya kulipa mafao ya kustaafu au kuacha kazi kwani katika sheria kikokotoo hakikuwekwa na Serikali ilisema kuwa formula itawekwa katika kanuni. Uzoefu unaonesha kuwa sheria nyingi zinazopitishwa na Bunge na kusainiwa na Mheshimiwa Rais zinachelewa kutungiwa kanuni. Hivyo basi, Serikali ijitahidi kutunga kanuni mapema ili sheria iweze kuwa effected.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali itoe elimu kwa wadau wa mifuko hii ili ku-raise awareness kuhusu mabadiliko ya sheria hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nachangia kwa niaba ya Mheshimiwa Selemani Zedi na jina langu lipo huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia Wizara hii ya Afya, napenda kuishukuru sana Serikali kwa Mkoa wangu wa Mwanza, wametupa shilingi bilioni tatu na tumeweza kufanyia ukarabati Vituo vya Afya zaidi ya saba kikiwemo Kituo cha Kahangara (Magu); Karume (Itemela), Kome (Buchosa); Kagunga (Serengema), Mallya (Kwimba), Lugeye (Magu) pamoja na Misungwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali kwa kuweza kutoa fedha hizi ili kuweza kuboresha huduma ya afya katika Mkoa wa Mwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena kuchangia katika suala la saratani ya shingo ya uzazi. Ni jambo jema kwamba Serikali sasa imeleta chanjo ili kuwachanja watoto wenye umri wa miaka 14. Naomba kuishauri Serikali kwamba sasa iangalie kwenda kwenye phase II ambayo ni ya watoto wa kike wenye umri wa kuanzia miaka 15 mpaka miaka 25. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kuishauri Serikali kuangalia ni namna gani wanaweza wakaanza pia na watoto wenye umri wa miaka tisa, kumi na kuendelea mpaka hiyo 14. Kwa sababu gani naishauri Serikali kufanya hivyo? Umri wa miaka tisa mpaka 14 watoto wetu sasa hivi wameanza kuingia katika masuala ya kujamiiana mapema sana. Ni vyema sana kuwakinga ili kuwaepusha kupata saratani ya shingo ya uzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, saratani ya shingo ya uzazi inaambukizwa kwa magonjwa ya kujamiiana. Kwa hiyo, nashauri sana watoto wetu kuanzia miaka 9 hadi 14 na wao pia Serikali iwaangalie ni namna gani wanaweza wakawapatia chanjo. Pia watoto wa kiume wanaweza wakapatiwa chanjo ya Gardasil pamoja na Gardasil 9 ambayo inaweza ikawasaidia kuwakinga watoto wa kike wasipate maambukizi ya kujiamiiana na hatimaye kupata saratani ya shingo ya uzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuongelea suala la ugonjwa wa myoma. Ugonjwa wa myoma ni ugonjwa ambao unawapata akina mama, wanapata uvimbe katika kizazi na inapelekea wanawake kutolewa kizazi na hatimaye kukosa watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali kuweza kusaidia kufanya utafiti wa ugonjwa huu kwamba upo kwa ukubwa kiasi gani? Kuna siku utakumbuka katika Bunge hili wanawake wote walisimamia kuchachamaa kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya wa kipindi hicho alisema ugonjwa huu siyo mkubwa na siyo hatarishi. Wanawake wote humu ndani walishangaa na wakanyanyuka. Ninaomba Serikali iweze kufanya utafiti wa ugonjwa huu wa myoma kwa sababu ni ugonjwa ambao unawamaliza sana wanawake, wanakosa watoto katika umri mdogo sana kuanzia miaka 25 hadi 35. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuongelea suala la utoaji huduma wa afya kwa akina mama wajawazito kuhusiana na suala la delivery packs. Serikali ilizitoa delivery packs bure kwa mwaka mmoja tu na baada ya hapo wanawake wengi tumekuwa tukiuliza maswali ndani ya Bunge na kujibiwa kwamba delivery packs zinakuja. Serikali cha kusikitisha sana delievery packs sasa tumeambiwa kwamba zinauzwa na bahati mbaya sana zinauzwa shilingi 21,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanawake huko vijijini hawana uwezo wa kununua hizi delivery packs kwa bei hiyo. Ninaiomba Serikali irudie kuangalia upya gharama za bei ya delivery packs angalau basi zishuke bei hadi kufikia shilingi 10,000. Kwa sababu kwenye pharmacy nyingine huko mjini wanauza shilingi 10,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la delivery packs siyo la muhimu sana. Tunatarajia mama mjamzito anapofika hospitali, kuna delivery kit ambapo nurse anapotoka kwenda kumhudumia huyu mama wakati anajifungua, anapoenda kufanya ile procedure, anaondoa vifaa vinavyohotajika kutoka kwenye delivery kit ili apate delivery pack aende kumsaidia yule mama aweze kujifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utaona hili suala la delivery packs sio la lazima sana Serikali kutoa bure, lakini waangalie ni namna gani wanaweza wakapunguza bei ili wale wanaoweza kununua waweze kununua.

Mheshimiwa Naibu naunga mkono hoja. Nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafsi hii ili niweze kuchangia katika Wizara ya Katiba na Sheria. Katika kuchangia Wizara hii ya Katiba na Sheria, naomba kuchangia kuhusiana na masuala ya utoaji haki kwenye Mabaraza ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabaraza ya Ardhi yalianzishwa kwa sheria ya mwaka 2002 Sura ya 114, lakini Mabaraza haya ya Ardhi yalianzishwa ili kuweza kusaidia kutatua migogoro mingi ambayo inajitokeza katika umiliki wa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabaraza haya yamekuwa yakikumbwa na changamoto mbalimbali. Changamoto mojawapo ni kwamba Wenyeviti wa Mabaraza haya ya Ardhi hawana uelewa wa kutosha kwa upande wa kisheria na hivyo kushindwa kuitatua vizuri migogoro ya ardhi na kusababisha wananchi kukosa haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia changamoto nyingine katika Mabaraza haya ya Ardhi ni kutokana na posho ambayo wanalipwa kwamba ni ndogo sana na wakati mwingine posho ambayo wanalipwa Wenyeviti hawa wa Mabaraza ya Ardhi inacheleweshwa. Kwa hiyo, inasababisha Wajumbe hawa wa Mabaraza ya Ardhi kukosa ari ya kufanya kazi vizuri na hivyo kusababisha kushindwa kutatua migogogro ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali kwamba ilete mabadiliko ya kisheria ili kuweza kufanya mabaraza haya ya ardhi kutokufanya kazi zake kwa sababu wameshindwa kufanya kazi zao katika kutatua migogoro ya ardhi. Kwa sababu hapo kabla, migogoro ya ardhi ilikuwa inatatuliwa katika mfumo wa kimahakama. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali iweze kufanya marekebisho ya sheria ili kurudisha kesi hizi za migogoro ya ardhi kufanyika katika mfumo wa kimahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu katika Mahakama, mawakili wetu hawa wanao uwezo mkubwa wa kisheria kuweza kutatua migogoro ya ardhi. Pia mawakili wanakuwa na maadili kiasi kwamba wana uwezo wa kutatua migogoro ya ardhi na hivyo kupunguza kabisa migogoro ya ardhi au kuimaliza kabisa katika nchi yetu ya Tanzania ambayo inaongoza pia katika Bara la Afrika katika akuwepo kwa migogoro ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la kesi la mirathi pamoja na kesi za ndoa. Wanawake wengi ndio wamekuwa waathirika katika kesi za mirathi pamoja na kesi za ndoa. Naishauri Serikali itusaidie kuleta sheria ya kuwa na Mahakama Maalum ambayo inaweza ikasikiliza kesi za mirathi pamoja na kesi za ndoa. Kwa sababu kutokana na jamii yetu sijui kubadilika au kupata uelewa mkubwa zaidi, sijui inakuwaje, migogoro ya mirathi na ndoa imekuwa ni mingi sana, imekuwa ikilundikana katika mahakama zetu. Tunafahamu kabisa tuna upungufu wa watumishi katika mahakama zetu na hivyo kufanya kesi kuludikana na kushindwa kufanyika vizuri. Kwa hiyo, naishauri Serikali kuleta sheria ili paweze kuanzishwa Mahakama Maalum ambayo itakuwa inasimamia kesi za mirathi pamoja na kesi za ndoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea suala la Uandishi wa Sheria kama inavyoonekana katika Kitabu cha Wizara ya Katiba na Sheria. Kwa muda wa miaka miwili na nusu nimekuwa ni Mjumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo.

Katika uchambuzi wa sheria ndogo tumekuwa tukiona makosa mbalimbali yamekuwa yakifanyika katika uandishi wa sheria ndogo. Makosa hayo yalikuwa ni makosa ya kiuandishi na makosa ya kikatiba. Cha kushangaza sana, tunao watendaji ambao ni wanasheria katika Halmashauri zetu ambao wanaziandika hizi sheria lakini bado makosa yamekuwa yakipatikana kwa takribani asilimia 60 katika sheria hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, hiyo inasababisha watu kunyimwa haki zao. Kwa sababu unakuta kabisa kama sheria inakiuka Katiba, moja kwa moja mtu atakuja kukosa haki yake. Hivyo basi, ninashauri pawepo na semina mbalimbali. Pamoja na kwamba Serikali inafanya jitihada mbalimbali, lakini naomba semina ziweze kufanyika katika Halmashauri zetu kwa wale wanasheria ili wafahamu namna ya uandishi mzuri wa kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninaomba Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ipewe uwezo, watumishi waongezwe na pia watumie teknolojia mpya katika uandishi wa kisheria ili kuepuka makosa mbalimbali ambayo yanatokea hususan katika uandishi wa sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sasa nijielekeze katika suala la kuomba mabadiliko ya sheria mbalimbali. Katika Bunge hili Waheshimiwa Wabunge, na mimi nikiwepo wa kwanza tumekuwa tukiomba mabadilko ya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 na Serikali imekuwa ikitoa ahadi mbalimbali, kuna siku nilisimama hapa tarehe 5 Mei,2016 nikiitaka Serikali kuleta mabadiliko ya Sheria ya Ndoa na Serikali ilitoa ahadi kwamba mwezi Septemba katika mwaka huo 2016 wataleta Muswada wa Mabadiliko ya Sheria ya Ndoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza sana, Serikali mpaka sasa imekaa kimya, ukiuliza kuhusiana na suala la sheria, wanaanza kusema mabadiliko ya Sheria ya Ndoa Serikali haina majibu sahihi, lakini hiyo ilIkuwa ni ahadi ya Serikali. Hivi tunataka kusema kwamba wananchi wasiiamini tena Serikali yao kwa sababu inatoa ahadi za uongo? Naomba tusifike huko, wananchi bado wanayo imani na Serikali. Kwa hiyo, ninaitaka Serikali kutimiza ahadi yake ya kuleta Muswada wa Mabadiliko ya Sheria hii ya Ndoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyoitaka Serikali, kuna sababu mbalimbali. Serikali baada ya kusema kwamba italeta huo Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Sheria ya Ndoa, hawakuleta. Matokeo yake, wanamitandao wametumia upenyo huu au wametumia mwanya huo kwenda kuishtaki Serikali mahakamani na hatimaye Serikali wakashindwa katika kesi hiyo. Mahakama ikatoa ruling kwamba kifungu cha 13 na 17 viondolewe kwa sababu vinaleta ubaguzi katika Sheria hii ya Ndoa. Serikali ikakata rufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kukata rufaa, mimi sitaki kuingilia muhimili wa Mahakama, mimi niko katika muhimili mwingine kabisa wa Kibunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabisa Serikali sasa iangalia na ione kwamba umefika muda muafaka, Watanzania wote wanataka Sheria ya Ndoa iweze kufanyiwa marekebisho kwa sababu watoto wetu wanateseka sana. Ukiangalia sheria hiyo, inaenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 12 (1) ambayo inasema: “Binadamu wote huzaliwa huru na wote ni sawa.” Vilevile
(2) inasema, “Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa.” Mtoto huyu wa kike naye anastahili kutambuliwa na kuheshimiwa na kupewa uhuru wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la usawa katika utaungwaji wa sheria, lakini sheria hii ya ndoa imetungwa kibaguzi, imeenda kinyume kabisa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano Tanzania. Ibara ya 13 inasema, watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ya ubaguzi wowote kulindwa na kupata haki mbele ya sheria, lakini sheria hii inambagua mtoto wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 kifungu cha 16 inatafsiri maana ya ndoa. Inasema, “Muungano lazima uwe wa hiari.” Sasa muungano huu unafanywa na wazazi, ndio wanaotoa ridhaa ya mtoto wa kike kuolewa chini ya umri wa miaka 18. Kwa maana hiyo basi, sheria hii ya ndoa iko kinyume, yaani yenyewe inaji- contradict yenyewe kwa yenyewe. Kwa maana hiyo, ninaitaka Serikali kuangalia vifungu hivyo ambapo vina contradiction yenyewe kwa yenyewa na pia na Katiba iweze kufanyia marekebisho sheria hii ya ndoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hapa nchini Tanzania, pamoja na makubaliano ya Kimataifa ambayo tumekuwa tukiyasaini, tunaenda kinyume kwa sababu gani? Hizi ndoa ambazo zinafungwa za hawa watoto ambao wako chini ya umri wa miaka 18 zinaenda kinyume na hichi kifungu cha 16. Kwa maana hiyo, sheria hizo zote ni batili. Kwa hiyo, ninaitaka Serikali kutoa tamko na kusema kuwa watoto walioolewa chini ya miaka 18, ndoa hizo ni batili na waweze kurudi katika kazi zao, waende wakasome waweze kuwa kama sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mngenipata mimi…
(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, naomba leo nianze kwa kutoa tafsiri fupi ya nini maana ya viwanda. Kiwanda ni mahali ambapo malighafi inachakatwa kuwa bidhaa iliyokamilika kwa ajili ya mtuamiaji au bidhaa kwa ajili ya viwanda vingine viweze kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa tafsiri hiyo fupi ya viwanda, sasa tutaona Tanzania tutaweza kuelekea katika nchi ya viwanda. Historia ya viwanda duniani kote ukiangalia kwa mfano Britain, America, India, France, China walianza kwa kuwa na viwanda vya nguo na ndipo wakaweza kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Zitto ameeleza kwa kifupi mimi nitaenda kwa undani zaidi. Inasikitisha sana ni kwa namna gani sisi kama Tanzania tunaweza kuwa ni nchi ya viwanda kama hatutaongelea viwanda vya nguo. Leo katika kitabu hiki cha Mheshimiwa Waziri sijaona ni namna gani ameongelea viwanda vya nguo nchini Tanzania. Hii inasikitisha sana kwa sababu inaonesha ni kwa namna gani hatuwezi kuwa na nchi ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kuwa na nchi ya viwanda nchini Tanzania halijaanza leo, lilianzishwa na Mheshimiwa Rais wetu Mtukufu, Hayati Julius Kambarage Nyerere mwaka 1970 hadi mwaka 1992 viwanda vikabinafsishwa. Inasikitisha Serikali haijaweza kuvichukulia hatua yoyote viwanda 156 vilivyobinafsishwa na havifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niko katika Kamati ya Viwanda na biashara. Kamati ilitisha list ya viwanda 156 ambavyo vilibinafsishwa mwaka 1992. Taarifa ambayo ililetwa mbele ya Kamati na ninayo hapa, Serikali inajaribu kueleza ni kwa namna gani inachukua hatua lakini ukiangalia maelezo yanayotolewa ni kwamba ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali unachukuliwa na wanasema mashauri mengi yako mahakamani.

Mheshimiwa Spika, taarifa hii kusema ukweli hata Kamati ilisoma na ikaona na haikuweza kuridhika na majibu ya Serikali. Nilitegemea leo hii katika kitabu hiki ambacho ni cha Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Waziri angeweza kuelezea na kufafanua ni kwa namna gani Serikali imejipanga kuwachukulia hatua watu ambao walibinafishiwa viwanda
156. Watu hawa ni wezi, ingekuwa ni nchi nyingine kama China wangenyongwa kwa sababu ndiyo wametufikisha hapa sisi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umasikini tulio nao Tanzania leo ni kwa sababu ya viwanda vilivyobinafishwa. Viwanda hivyo 156 vingi ambavyo ni vikubwa vilikuwa ni vya nguo. Sasa ukiangalia kama nilivyoanza kusema viwanda vya nguo vilisababisha nchi za Marekani, Britain, France na China kuweza kufanikiwa kuwa nchi za viwanda lakini leo hii sasa sisi Tanzania tuko wapi, tunaenda wapi? Naitaka Serikali kuchukua hatua kwa hivi viwanda ambavyo vilibinafsishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutangulia kusema hayo, naomba sasa tuangalie katika Mkoa wa Mwanza. Mwanza tuna Kiwanda cha MWATEX. Kiwanda cha MWATEX kilikuwa kina wafanyakazi zaidi ya 3,500 miaka ya nyuma kikashusha wafanyakazi hadi kufikia 1,500. Leo hii tunaongelea wafanyakazi si zaidi ya 150 katika Kiwanda cha MWATEX. Suala hili linasikitisha sana. Siku moja nilisikia Mheshimiwa Rais akisifia kwamba Kiwanda cha MWATEX kinafanya vizuri, yawezekana Mheshimiwa Rais hajapata ukweli kutoka kwa watendaji juu ya Kiwanda cha MWATEX. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana sana, watendaji wa Wizara hii ya Viwanda wamsaidie Mheshimiwa Rais, kwa kumueleza ukweli na si kwa kuja hapa kwa kujitamba kwamba tuna viwanda vingi, viwanda vingi wakati impact kwa Watanzania haionekani? Mtu anakuja hapa anaongelea suala la viwanda vya cherehani, hivi unataka kusema leo hii mimi nikimuita Waziri wa Viwanda na Biashara kwamba twende naye Mwanza tukazindue viwanda watu wana vyerehani vinne, atakuja kweli? Je, inaleta impact? Mimi hainiingii akilini, sahamahi sana kwa kusema hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna Kiwanda cha MUTEX ambacho kiko Musoma kimekufa. Pamoja na viwanda vingine ambavyo vimekufa Kiwanda hiki cha MUTEX kinanisikitisha kwani kilikuwa kinatoa vitenge na kanga nzuri, vitenge vilikuwa vinauzwa mpaka nje ya nchi Swaziland. Leo hii kiwanda kimekufa lakini katika kitabu kiwanda hiki hakionekani kuongelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naitaka Serikali kuangalia ni kwa namna gani inachukua hatua madhubuti za mikakati kuweza kuviinua viwanda ambavyo vilikuwa vimekufa ambavyo ni viwanda vya nguo ili nasi tuweze kuitumia pamba yetu. Katika Mkoa wa Mwanza na mikoa mingine kama Simiyu na Shinyanga wanalima pamba kwa wingi lakini unapoangalia kwenye taarifa ya Waziri ni asilimia 30 tu ya pamba ndiyo ambayo inatumika, pamba nyingine yote inaenda nje.

TAARIFA . . .

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuweza kunisaidia kujibu taarifa ile isiyokuwa na maana yoyote. Kwa sababu mimi sijasema viwanda ameviua Mheshimiwa Mwaijage ndiyo maana naona kwamba taarifa ya kaka yangu pale haijakaa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini naomba niendelee kwa kusema kwamba viwanda hivi vinapaswa kufufuliwa kwa ari kubwa sana ili pamba iweze kutumika kwa asilimia walau 70 ndani ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Urafiki kinasikitisha. Leo hii ukienda kwenye kiwanda kile kuna show room ya magari ya Wachina iko pale. Ni kwa sababu gani Kiwanda hiki cha Urafiki hakifanyi kazi? Tunakuomba Mheshimiwa Mwaijage pamoja na watendaji wote katika Wizara hii muangalie viwanda hivi ambavyo ndivyo vinaweza kutusaidia Watanzania kujivunia na kuwa nchi ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii ukiangalia Kiwanda cha Kiltex, Mbeya Textile, Sungura Textile, Tabora Textile vyote havipo. Katika taarifa tunaambiwa kuna viwanda 11 vya nguo, sijui ni viwanda gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na yote hayo niliyoyaongea, naomba nitumie dakika mbili kutoa ushauri kwa Serikali. Hatuwezi kuwa na viwanda vya uhakika kama hatuwezi kusaidia upatikanaji wa uhakika wa umeme katika viwanda vyetu. Mashine nyingi zinakufa katika viwanda kwa sababu umeme upatikanaji wake siyo effective. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Serikali iweze kujitahidi kuangalia viwanda vyetu vinapata umeme wa uhakika lakini pia vinapata maji ya uhakika na pia barabara za kutoa malighafi sehemu moja kupeleka katika viwanda na kutoa bidhaa viwandani kwenda sehemu za masoko ili kuweza kusaidia viwanda vyetu kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba kutoa ushauri, kama inawezekana Serikali ichukue ushauri huu, kwamba viwanda vya nguo vitolewe ile asilimia 18 ya kodi ili kuweza kuvi- motivate kuweza kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja lakini yale niliyoyasema yaweze kuzingatiwa na Serikali na hatimaye yaweze kufanyiwa kazi. Nashukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika kujadili Taarifa ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba kupongeza juhudi za Serikali za awamu zote kwa kuhakikisha kuwa nchi yetu inakuwa ni nchi ya uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sababu iliyopelekea nchi yetu kubinafsisha viwanda ni kuleta tija. Kama nchi, tuliamini ya kwamba kubinafsisha viwanda kutaleta tija, kuongeza uzalishaji, pia kuongeza ajira, kuweka teknolojia mpya, kuongeza ubora na thamani ya bidhaa ambazo zinazalishwa katika viwanda hivyo tulivyovibinafsisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaendelea kuamini kwamba viongozi waliopita walikuwa na nia njema ya kubinafsisha viwanda vyetu. Ila nia hiyo njema iliharibiwa na baadhi ya Watendaji na Wawekezaji ambao walikuwa na dhamira ya kupotosha dhamira kubwa ya kubinafsisha viwanda ambavyo vilikuwa vimebinafsishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulibinafsisha viwanda yapata 156, lakini leo hii viwanda vinavyofanya kazi na hata taarifa ya Kamati inaonyesha ni viwanda 16 tu peke yake katika viwanda 156. Suala hili siyo suala la kulifumbia macho, lakini kwa sababu tumeshateleza, hatuna budi kuendelea kuishauri Serikali ili kuona ni kwa namna gani wanaweza wakarudisha nia ya madhumuni ambayo yalikuwa ni mema ya ubinafsishaji wa viwanda hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali katika maeneo mawili; eneo la kwanza, kuhakikisha ya kwamba inapitia mikataba yote ambayo ilihusika katika ubinafsishaji wa viwanda. Wakati zoezi zima la ubinafsishaji wa viwanda linafanyika, kulikuwa kuna mikataba ambayo ilikuwa ni ya ovyo, mikataba ambayo iliifanya Serikali kutokuwa na nguvu ya kuweza kuwanyang’anya viwanda wale ambao walivitumia vibaya na kuweza kuvirudisha kwa wale ambao sasa wana uwezo wa kuvifanya viwanda hivi kuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, naishauri Serikali, kama itampendeza Mheshimiwa Spika kuunda Kamati Maalum ya Kibunge ili waweze kufuatilia mikataba ambayo Serikali iliingia na ili kuweza kuipa Serikali nguvu ya kuweza kuvitwaa viwanda ambavyo havifanyi kazi kama vile unavyoona kwamba katika viwanda 156 ni viwanda 16 peke yake ambavyo vinafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, naishauri Serikali kuangalia namna ya kuviondoa katika orodha ya viwanda, viwanda vile ambavyo havifanyi kazi. Hii ni kwa sababu ukiangalia kwenye taarifa yetu ya Kamati; na Kamati imesisitiza kwamba vile viwanda ambavyo havifanyi kazi vizuri viondolewe basi kwenye orodha ili kuepuka mgongano wa mawazo wa kusema kwamba tuna viwanda vingi na vinafanya kazi, tukiendelea kuamini kwamba vinafanya kazi wakati havifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili kuondoa hiyo notion ya kuwafanya Watanzania waamini kwamba tunavyo viwanda vikubwa na vingi ambavyo vinafanya kazi, ni vyema tukaondoa vile viwanda ambavyo havifanyi kazi katika orodha ya viwanda ambavyo vimebinafsishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuangalia katika suala zima la upelekaji wa fedha. Katika taarifa ya Kamati tumeona upelekaji wa fedha katika Wizara ya Viwanda na Biashara wamepelekewa fedha kwa asilimia 18 hadi kufikia Desemba, 2018. Katika hiyo asilimia 18, ni 6% peke yake ambayo ilikuwa imeenda kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini nia njema ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ambayo anatangaza kila mara kwamba anataka kuona uchumi wa viwanda katika nchi yetu ya Tanzania. Ninaamini Mheshimiwa Rais anayo nia njema kabisa, lakini je, nia njema aliyonayo Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, itafikiwa vipi kama tu hata upelekaji wa fedha katika Wizara ni kwa asilimia ndogo namna hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kuangalia kwamba kama tunataka kweli kwenda katika uchumi wa viwanda, tuhakikishe tunatenga fedha za kutosha lakini zile fedha tunazozitenga tuhakikishe zinaenda kama ilivyoidhinishwa na Bunge ili kuweza kusaidia kuleta tija katika suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Wizara ya Mazingira, ninaamini kwamba ni Wizara nyeti, ina mambo mengi sana ya kuyaangalia. Kwa mfano, katika hiki kipindi cha hivi karibuni, maeneo mengi sana yanaonekana kwenda kuwa na jangwa na kuna uharibifu mkubwa sana wa mazingira, lakini Wizara hii imekuwa ikitengewa fedha ndogo; na hizo fedha kiasi kidogo ambacho kinatengwa pia kinaenda kidogo. Kwa maana hiyo, Wizara hii tunaizorotesha na kuifanya ishindwe kufanya kazi yake ya kuweza kuyatunza mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa siku ya leo baada ya kuyasema hayo, ninaomba Serikali iweze kupitia maoni ambayo yametolewa na Kamati ya Viwanda na Biashara, lakini pia niendelee kupongeza juhudi ambazo zinafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano ili kuhakikisha kwamba tunafikia katika uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili nami niendelee kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu. Pia niendelee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunijalia afya njema ili niweze kutoa michango yangu katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoanza kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI na Utawala Bora, naomba kuanza kwa kusema kuwa mwanazuoni mmoja ametafsiri viongozi wa kisiasa kuwa ni muhimu sana katika mamlaka za Serikali na hufanya maamuzi sahihi yanayoweza kuleta manufaa zaidi katika ustawi wa Taifa na watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeamua kuanza kwa kusema hivyo nikiamini kwamba sisi kama Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tukiwa kama viongozi wa kisiasa tunalo jukumu la kuhakikisha kuwa tunaishauri Serikali, tunaisimamia vyema ili kuhakikisha ustawi wa Taifa letu pamoja na wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa sababu yeye ameonyesha mfano wa yale ambayo nimeyatangulia kuongea, akiisimamia nchi yetu ya Tanzania kuhakikisha kwamba Watanzania wanaongozwa vizuri katika sehemu ya Utawala Bora lakini pia Watanzania wanaweza kupata ustawi na maendeleo katika nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI nikianza na suala la ujenzi wa vituo vya afya, pamoja na hospitali. Serikali imejitahidi sana kujenga na kukarabati vituo vya afya na hospitali, hiyo yote ni katika kuhakikisha inaboresha huduma za afya katika maeneo mbalimbali hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Mkoa wa Mwanza tumefaidika katika ukarabati na ujenzi wa vituo vya afya kama ambavyo imekuwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini, Mkoa wa Mwanza tumepata takribani shilingi bilioni 10.3 ambayo imetusaidia kurekebisha vituo vya afya katika maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza vikiwemo Wilaya ya Ukerewe, Wilaya ya Kwimba, Wilaya ya Magu, Wilaya ya Misungwi na Wilaya nyingine zote Mkoa wa Mwanza zimeweza kufaidika kwa kupata vituo vya afya na hospitali za wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi hizo za Serikali, zipo changamoto mbalimbali ambazo zinatokea katika jamii yetu. Maeneo kama ya visiwani, bado hawajaweza kupata huduma za afya kwa sababu wanatembea umbali mrefu na ukiangalia Mkoa wa Mwanza ni Mkoa umezungukwa na visiwa vingi. Kwa maana hiyo, wananchi wanapata changamoto ya usafiri kuweza kufikia huduma za afya kwa ukaribu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, ukiangalia Wilaya ya Ukerewe na Wilaya ya Ilemela, kuna Visiwa vya Irugwa Kisiwa cha Bezi. Wananchi ambao wanahishi katika visiwa hivyo ambavyo nimevitaja bado wanapata changamoto ya kufikia huduma huduma za afya. Ombi langu kwa Serikali, naiomba Serikali katika bajeti yake hii waweze kutenga fedha kwa ajili ya kutengeneza kujenga vituo vya afya katika maeneo hayo ya visiwani ili wananchi waweze kuzifikia huduma za afya kwa ukaribu na hatimaye kuweza kuokoa maisha ya wananchi, hususani tukiwalenga kundi maalum ambalo ni akina mama na watoto ili kuweza kupunguza vifo vya akina mama na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Mwanza pia tunayo Hospitali ya Ukerewe ya Wilaya ambayo ipo pale Nansio. Hospitali hii ya Wilaya ya Ukerewe inawahudumia wananchi wengi sana kutoka maeneo ya visiwani kule Ukerewe. Sasa kuwapunguzia wananchi kutoka Ukerewe kwenda kupata tiba au kwenda kupata huduma za kiafya za kibigwa, ninaishauri Serikali kuweza kukarabati Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe ambayo ipo pale Nansio. Hii itawasaidia wananchi wanaotaka huduma maeneo yale kwani hawapati huduma za kibigwa za kiafya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, naiomba Serikali iweze kutenga fedha katika kipindi hiki cha bajeti ili kuhakikisha kwamba hospitali hii ya Wilaya ya Ukerewe ambayo inahudumia wananchi wengi iweze kutoa huduma za Kibigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuchangia katika suala la elimu. Pamoja na juhudi za Serikali kujenga madarasa na shule za mabweni katika maeneo mbalimbali, bado tunazo changamoto kwa watoto wetu wa kike ambao wanatembea mwendo mrefu kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kupata elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtoto wa kike anapotembea mwendo mrefu, njiani anakutana na vikwazo mbalimbali. Atakutana na madereva wa bodaboda watamshawishi kupanda usafiri ili aweze kufika haraka shuleni. Atakutana na watu tumezoea kuwaita mashunga dadys, wataweza kumrubuni mtoto wa kike na kukatisha masomo yake hatimaye aweze kupata ujauzito ama la aolewe akiwa bado ni mdogo na hatimaye kukatisha ndoto zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi za Serikali kufanyika, lakini bado tunayo changamoto ambapo sehemu mbalimbali ambazo ziko mbali na maeneo ya shule za msingi, zinazo-feed shule zetu za Kata za Serikali kwa wanafunzi kutembea mwendo mrefu. Tunaishauri Serikali iweze kujenga shule za mabweni katika shule zetu za kata ili iweze kuwasaidia watoto wa kike wasiweze kutembea mwendo mrefu kwenda kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Mkoa wa Mwanza, sisi tunazo baadhi ya shule hapa ambazo nitazitaja ili Serikali iweze kuzisaidia. Kwa sababu nimeona katika ukurasa wa 124 katika kitabu hiki cha Wizara ya TAMISEMI wamesema kwamba watajenga shule za mabweni kwa kupitia EP4R. Kwa hiyo, naomba katika mpango huo shule hizi ikipendeza ziweze kuingia katika mpango huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule ya Bwisia ambayo iko Wilayani Ukerewe, Shule ya Sekondari Bujiku Sakila ambayo ipo Kwimba, Shule ya Sekondari Kabila ambayo ipo Wilayani Magu na Shule ya Sekondari Nyamadoke ambayo ipo Buchosa. Sehemu hizi zote ambazo nimejaribu kuziainisha, wanafunzi wanatembea zaidi ya kilomita tano kwenda kutafuta elimu. Hivyo, naamini kabisa kwa kufanya hivyo, wanafunzi wa kike wataweza kufaidika na hatimaye kufikia ndoto zao kama sisi wengine tulivyoweza kuzifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kuongelea suala la asilimia kumi ambalo linatakiwa kutenga na Halmashauri zetu kwa mujibu wa sheria ambayo tulipitisha wenyewe hapa Bungeni kuhusiana na wanawake ambao wanapata asilimia nne, vijana ambao wanapata asilimia nne na asilimia mbili inatakiwa kutolewa kwa watu wenye ulemavu. Kwa bahati mbaya sana baadhi ya Halmashauri zetu hazitimizi sharti hili la kutenga hii asilimia kumi. Nafahamu kabisa kwamba Halmashauri mbalimbali zinapata changamoto ya mapato kuwa ni madogo lakini kwa sababu hiki kitu kimewekwa kisheria, ninaamini wanatakiwa kuzitenga fedha hizi. Kwa bahati mbaya fedha hizi hazitengwi, matokeo yake, hata viongozi wakubwa wanapokuja kutembelea katika Majimbo yetu, taarifa ambazo wanazopatiwa siyo za ukweli. Kwa mfano, wanaambiwa Halmashauri imetoa shilingi milioni 500, unajiuliza swali, hivi katika Halmashauri kwa mfano ya Jiji, hiyo ndiyo fedha pekee iliyopatikana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali kuhakikisha wanafuatilia Halmashauri ambazo hazitengi fedha hizo za asilimia kumi ili waweze kuzitenga na kuweza kuwasaidia wananchi.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako mzuri.

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kupitia taasisi mbalimbali zinazotoa matibabu ya kibingwa. Pia nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara ya Afya kwa ushirikiano wao kwa Waheshimiwa Wabunge katika kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu afya ya uzazi, mama na mtoto; Serikali imejitahidi sana kujenga zahanati na vituo vya afya na hivyo kupunguza mwendo mrefu wa wananchi pamoja na kinamama wajawazito ili kufikia huduma za afya, lakini bado vifo vya mama na mtoto idadi ipo juu hususan akina mama wajawazito ambapo takwimu zinaonesha kuwa akina mama 24 wanafariki kila siku wanapokuwa wanajifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, vifo vingi hutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kutokwa na damu nyingi wakati wa kujifungua, kutokufanya maamuzi ya njia za kujifungua mapema kama vile upasuaji, ukosefu wa dawa aina ya misoprostol and oxytocin hususan vijijini na pia ukosefu wa vifaa tiba na wataalam wa kutosha katika vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, suluhisho ni kwamba Serikali iweke mkakati wa kuajiri Community Health Workers na wasambazwe maeneo yote hususan katika zahanati na vituo vya afya vya vijijini ili waweze kutoa huduma za afya na elimu kwa akina mama wajawazito. Ni vyema Serikali itenge fedha kwa ajili ya kukabiliana na vifo vya mama na mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, naomba Serikali iharakishe mchakato wa kuleta sheria ya Universal Health Coverage ili kuwezesha wananchi wote wapate huduma bora za afya kwa usawa. Pia Serikali ijitahidi kutafuta wafadhili ili kusambaza vifaa kwa ajili ya kuanzia kusajili wananchi na huduma ya NHIF iliyoboreshwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu tunapoelekea katika kuazimia azimio hili la Minamata Convention.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa bila kupoteza muda naipongeza Serikali kwa kuleta azimio hili ndani ya Bunge. Ukiangalia umuhimu mkubwa wa kuridhia Azimio la Minamata; Minamata kwanza yenyewe kama jina la convention yenyewe imetokana na madhara ambayo yaliwapata nchi ya Japan katika hilo eneo ambalo linaitwa Minamata. Madhara ambayo yalitokana na disposal ya hii sumu ya zebaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sasa nchi kama Tanzania na sisi kuweza kuridhia mkataba huu kwa ajili ya kuweza kulinda afya za wananchi hususan wachimbaji wadogowadogo katika migodi ya dhahabu ambao ndio watumiaji wakubwa sana wa zebaki katika uchenjuaji wa dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona wananchi wengi sana hususan Kanda ya Ziwa ambako ndio kumezungukwa na migodi mingi wakipata athari za sumu inayotokana na zebaki kwa ajili ya kuchenjua dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea Kanda ya Ziwa, kule kina mama wanajifungua watoto wenye vichwa vikubwa, kule ndio tunaongoza kwa tatizo hilo. Hatujaishia hapo, kule Kanda ya Ziwa wakina mama ndio wanaongoza kwa kupata watoto ambao wanakuwa na ulemavu wa viungo mbalimbali kwenye mwili. Kwa hiyo, ukiangalia ukubwa wa tatizo hili ni jambo zuri sana Serikali imeona kwamba ilete azimio hili ili sisi kama Bunge tuweze kuliridhia na hatimaye kupata faida mbalimbali katika kuridhia mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nchi Tanzania tutapata faida zipi, moja; tutapata faida ya kwamba tunaweza tukapata mbadala wa matumizi ya zebaki. Kama tumeona kwamba zebaki ina matatizo ambayo yanasababisha matatizo ya kiafya kwa wananchi hususan hawa wachimbaji wadogo wadogo, ina maana kama nchi tunaporidhia mkataba huu, tutapata faida ya kupata mbadala wa matumizi ya zebaki, kwanza kwa sababu katika nchi zote ambazo zimeridhia mkataba huu kutakuwa na mambo matatu ambayo yatafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza, ni kuweza kupunguza matumizi ya zebaki katika kuchenjua dhahabu kwenye migodi. Lakini kitu kingine ni kwamba ni nchi zote ambazo zimeridhia mkataba huu zitazuiwa kuchimba hii zebaki. Sasa kama zile nchi ambazo zinachimba zebaki zitazuiliwa sisi kama Tanzania tusiporidhia mkataba huu tutajipanga vipi kupata matumizi mbadala ya zebaki kama zebaki itakuwa imezuiliwa. Kwa hiyo, utaona ni vizuri kama nchi tukaridhia mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nina jambo moja la kushauri Serikali pamoja na kwamba tunaenda kuridhia mkataba huu ninaomba wazingatie article 18 ambayo inazitaka nchi zilizoridhia Mkataba huu kutoa elimu kwa watumiaji wa zebaki, lakini pia kuhakikisha kwamba inawasaidia wananchi kufahamu ni madhara gani wanayapata katika utumiaji wa zebaki. Naomba Serikali iweke mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba wanatoa elimu kwa wananchi ambao wanaathirika na zebaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia naiomba Serikali izingatie article 16 ambayo inazitaka nchi ambazo zimeridhia huu mkataba kuhakikisha wanatoa huduma bora za kiafya kwa zile sehemu/yale maeneo ambayo wameathirika na matumizi ya zebaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo naomba Serikali waweke mpango mkakati kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yameathirika kutokana na matumizi ya zebaki wanapata huduma bora za kiafya ili kuweza kuwasaidia wananchi ambao tayari wamekwisha kuathirika, lakini pia ninaiomba Serikali kuzingatia ushauri huu katika mkataba huu wa zebaki umeweka kipengele ambacho kipo katika article 26 ambayo inazitaka nchi kuomba waweze kufanya amendment katika mkataba huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tusijifunge, katika mkataba huu matumizi yamewekwa kwamba kuacha kutumia ndani ya miaka kumi na tano, kwa hiyo naomba Serikali izingatie article 26 ili waweze kufanya amendment kupunguza muda wa matumizi ya zebaki ili kuweza kuwaokoa wananchi wetu. Ahsante na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. ZAWADI K. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuendelea kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitachangia kwa utaratibu kabisa ili labda Wizara kupitia Waziri mwenye dhamana pamoja na Naibu Waziri wake waweze kunisikiliza kwa umakini na kuweza kupata kile nilichonacho kuhusu viwanda na biashara katika nchi yetu hii ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza kwa kusema kwamba kama kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa lolote lile, basi viwanda ni nguvu na kichocheo cha maendeleo ya uchumi katika Taifa lolote lile. Ili tupate mapinduzi ya viwanda pamoja na kilimo tunahitaji kuwa na teknolojia ya kisasa ili kuweza kuleta tija katika uzalishaji wa kilimo pamoja na uzalishaji wa viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika nchi yetu ya Tanzania mpaka sasa tumeshindwa kufungamanisha kilimo pamoja na viwanda. Mheshimiwa Rais anayo nia njema sana anaposema anahitaji kuona Tanzania ya viwanda ili kuweza kuufikia uchumi wa kati. Sijui ni wapi tunakwama hadi tunashindwa kufikia yale malengo na azma njema ambayo viongozi wetu waliopita na waliopo sasa wamekuwa wanayo toka enzi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara, pamekuwepo na mapungufu ama changamoto ya upatikanaji wa fedha. Mimi naomba nijikite katika fedha za maendeleo. Fedha za maendeleo katika Wizara hii ya Viwanda na biashara kwa mwaka 2018/2019 imepelekwa kwa asilimia 6.48 tu. Swali tu la kujiuliza sisi kama Waheshimiwa Wabunge, kweli tunaweza tukaifikia azma ya Mheshimiwa Rais ya nchi ya viwanda na kutupeleka kwenye uchumi wa kati? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo taasisi mbalimbali katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara ambazo zingeweza kusaidia uchochezi wa kuwa na kilimo cha kisasa na tekonolojia ya kisasa katika viwanda vyetu nchini Tanzania. Tunazo Taasisi kama vile TEMDO, CAMARTEC, TIRDO pamoja na SIDO. Nikiwa kama Mjumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara, Kamati ilikwenda kutemebelea miradi hii ya taasisi hizi ambazo nimezitaja, cha kusikitisha sana tulivyofika katika taasisi hizi hakuna fedha hata shilingi moja ambayo ilikuwa imeenda kwa mwaka wa fedha 2018/2019. Zaidi Kamati ilifika pale na kukuta kwamba yale machache ambayo yamefanyika na ambayo ni mazuri yametumia fedha kiasi kidogo tu ambacho kilipelekwa kwa mwaka wa fedha 2017/ 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, naomba niwapongeze watumishi wote ambao wanafanya kazi katika Taasisi za TEMDO, TIRDO pamoja na CAMARTEC. Watumishi hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu lakini wameweza kujitoa katika kuhakikisha wanalisaidia Taifa hili na kumsaidia Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba azma ya viwanda inakwenda kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia katika ukurasa wa 72, 73, 74 na 75 Mheshimiwa Waziri amejinadi na kujieleza pale kwamba hizo taasisi za TEMDO, TIRDO na CAMARTEC ni namna gani zinaenda kutekeleza wajibu wake. Huo ndiyo mkakati ambao ametueleza katika kitabu chake lakini cha kusikitisha hajaweka mikakati, kama taasisi hizi hazipokei fedha unatarajia haya ambayo umeyaandika katika kitabu hiki Mheshimiwa Waziri yatatekelezwa vipi kama si kwamba unatutaka sisi kuziwekea lawama taasisi hizi lakini fedha hawana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua nitakuwa nimeongea kidogo kwa sauti iliyokuwa juu, lakini naamini kwamba ninaeleweka vizuri ninapoenda kuongelea suala hili. Kamati ilipotembelea katika taasisi zile tumekuta mambo ambayo kwa kweli yalitudhoofisha sana na tulijiona kuwa kama Kamati tumepelekwa pale kwenda kufanya nini kama sio tu kupoteza muda na kuchezea pesa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Taasisi ya CAMARTEC mishahara inayolipwa ni mikubwa ukilinganisha na mapato ambayo yanapatikana. Uzalishaji uliopo ni mdogo ukilinganisha na mishahara mikubwa ambayo inalipwa katika taasisi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mwaka 2016/ 2017, ililipwa shilingi milioni 900 ya mishahara ilhali mapato ya ndani ya mwaka huo yalikuwa ni shilingi milioni 242. Hiyo, haikutosha, mwaka 2017/2018 zimelipwa pesa milioni 864 wakati mapato ya ndani yalikuwa ni shilingi milioni 253. Mwaka 2018/2019 hadi kufikia mwezi Machi wamelipa mishahara shilingi milioni 362 wakati mapato yake hadi kufikia mwezi Machi ni shilingi milioni 214. Kwa trend hii siamini kama kweli tutaweza kufikia Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Serikali kuhakikisha kwamba wanachukua ushauri wa Kamati ambao imeutoa kuangalia taasisi hizi zinaenda kuwekwa chini ya management moja. Taasisi zinapokuwa under one management itaweza kuangalia sasa hivi pesa ipelekwe wapi na kufanya nini. Pia wale wafanyakazi ambao wameajiriwa katika zile taasisi wanakuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nijielekeze katika suala la Electronic Tax Stamp. Naamini mfumo huu wa ukusanyaji kodi kielektroniki umelenga kuwabaini wale ambao sio waaminifu katika ulipaji kodi. Ni suala zuri na mimi naipongeza Serikali kwa kubuni mfumo huo. Hata hivyo, gharama zile ambazo zinatumika kwa ajili ya ku-collect ile tax kwa wafanyabiashara ni kubwa sana. Kwa mfano, kijoti kile cha juice ya Azam, pact moja inatakiwa kulipa kodi ya Sh.3 lakini katika mfumo huu wa Electronic Tax Stamp gharama ya ku-collect ile Sh.3 ni Sh.9. Hebu angalia tunatumia Sh.9 kukusanya kodi ya Sh.3, hivi kweli inaingia akilini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali watakapokuja ku-windup watusaidie kutuambia ni mfumo gani ambao ulitumika kumpata huyu mwekezaji ambaye aliuweka huu mfumo. Hata Kamati wamesema pale kwamba, huu mfumo hauna teknolojia ambayo unaweza kusema kwamba it is a rocket science. Mfumo hata wewe binafsi unaweza ukaubuni. Kwa nini TRA haikufikiria kuwekeza wao wenyewe katika mfumo huu na kuleta mwekezaji? Naishauri Serikali iweze kukaa na huyu mwekezaji ili waweze ku-review zile gharama za kukusanya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya bajeti kuu ya Serikali. Nianze kwa kusema kuwa, natambua zipo sekta mbalimbali zinazochangia katika ukuaji wa uchumi wa wananchi na pato la Taifa, zikiwemo sekta za madini, mawasiliano, fedha, kilimo na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya kilimo ndiyo inachangia kwa asilimia kubwa na kutoa ajira kwa wananchi kwa wingi na hivyo kuondoa hali ya umaskini kwa wananchi. Hivyo basi, ni vyema Serikali ikawekeza kwenye kilimo kwa kutenga bajeti ya kutosha, bajeti ikiwa ni kubwa, mambo yafuatayo yataweza kutekelezwa:-

(a) Kufanya tafiti ya ardhi gani inafaa kwa zao lipi katika kila mkoa;

(b) Kufanya tafiti ya mbegu bora ili kuongeza uzalishaji ulio bora;

(c) Kuajiri Maafisa Ugani ili watoe elimu kwa wakulima ili walime mazao yenye viwango vya juu kwa ajili ya export na viwanda vya ndani; na

(d) Kuwekeza kwenye Taasisi ya Zana za Kilimo - CAMARTEC ili kukuza kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiweza kuwekeza kwenye kilimo ndipo viwanda na sekta zingine zitakua.
The Finance Bill, 2016
kunipa nafasi hii ili niweze kuendelea kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu. Katika kuchangia Muswada huu wa Fedha (Finance Bill) naomba kutoa tu ushauri kidogo kwa Serikali kama itaweza kuzingatia. Kuna haya mapendekezo ambayo yametolewa ya kurekebisha hii kodi ya usajili wa namba binafsi kutoka milioni tano hadi milioni kumi. Naamini kabisa kwamba lengo la Serikali lilikuwa ni zuri, kwamba ina lengo la kukusanya mapato na kuyaongeza zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napata wasiwasi kidogo, kwa sababu gani napata wasiwasi. Ukiangalia wakati kodi hii ilikuwa ni milioni tano watu ambao waliweza kusajili namba zao binafsi ni wachache sana, japokuwa sina data kamili, lakini naamini kwamba watu walikuwa ni wachache na wanahesabika na wanafahamika. Kwa hiyo basi, utaona kwamba, sasa hivi tunaposema kwamba, tuongeze kodi hadi kufikia milioni 10 napata shida kwamba inawezekana tukapoteza hata hawa ambao tayari walikuwa wanachangia katika kupata mapato.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi ni ombi langu tu kwa Serikali kwamba, waiache hiyo milioni tano. Nasema hivi kwa sababu gani? Milioni tano hii itakapobaki kwa muda wa miaka mitatu kila Mtanzania ambaye anaona kwamba kwa sababu hii ni luxury kwamba gari lako unaweza ukalisajili kwa bei ile ambayo imependekezwa kwa sasa hivi ya laki mbili na elfu hamsini, , lakini kama umeamua kusajili kwa kutumia jina lako mimi kama Kiteto, unaponiambia nilipe milioni tano kwa miaka mitatu, naona ni nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia inawezekana watu wengi sana watakapopatiwa elimu au matangazo yatakapokuwa yakipelekwa kwenye vyombo vya habari kwa kutumia chombo chetu cha TRA, basi unaweza kukuta watu wengi wataendelea kuhamasika ili kuweza kusajili hizo plate number za binafsi, lakini tunapopeleka kuwa milioni 10, nina wasiwasi kwamba mapato haya yatapungua kwani hawa ambao tayari walikuwa wamekwisha kujiandikisha, baada ya miaka mitatu kwisha wataamua kuachana na hilo suala na hapo Serikali itapoteza mapato yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kuchangia suala la kodi ya usajili wa pikipiki. Tunafahamu kabisa kwamba suala la pikipiki limesaidia vijana wengi kujipatia ajira. Wako watu wengi ambao wanajiweza wananunua pikipiki nyingi na kuwapatia vijana wetu kwa njia ya mikopo, hawa vijana wanakuwa wanalipa kidogo kidogo na hatimaye kuweza kuzimiliki hizo pikipiki. Kwa maana hiyo kodi ambayo sasa inapendekezwa kuongezwa kodi ya usajili kutoka 45,000 hadi 95,000, napata wasiwasi kwamba hawa bodaboda tutakuwa tumewaondolea hizo ajira. Kwa sababu atakapotokea mfanyabiashara mkubwa ananunua pikipiki anataka kuwapatia hawa vijana ili waweze kufanyia biashara na kulipa kidogo kidogo, wanatakiwa kwenda kuisajili, kwa hiyo bei ya kodi ya sh. 95,000, ina maana hawa vijana watakaposhindwa, Serikali itapoteza mapato katika eneo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naomba niishauri Serikali iweze pia kuendelea kulitazama suala hili, kama nia yetu ni kuendelea kukusanya mapato lakini bila kuwaathiri hawa vijana kwa kuwanyima ajira, basi naishauri Serikali ifuate ushauri ambao umetolewa na Kamati ya Bajeti kwamba kuiacha kodi ile kuwa hiyo hiyo sh. 45,000. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa siku ya leo kwa sababu ya swaumu, naomba niishie hapo na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kukubali kunipatia tena nafasi hii ili niweze kutoa michango yangu katika Bunge lako Tukufu. Kipekee kabisa ninaomba nikushukuru wewe binafsi kwa namna ambavyo unakuwa ukiwasaidia Waheshimiwa Wabunge na kuwaonesha moyo wa ubinadamu pale wanapokuwa wanapatwa na matatizo mbalimbali hususani ya msiba.

Mheshimiwa Spika, katika hili ninakushukuru wewe, Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Mawaziri na Waheshimiwa Wabunge wote ambao mliungana pamoja nami kipindi chote ambacho nilimuuguza baba yangu mpendwa na hatimaye Mwenyezi Mungu akampenda zaidi, lakini mlikuwa pamoja nami kwa kunifariji, mmenifariji sana na Mungu awabariki sana, ninawaombea kila la kheri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya salamu hizo za utangulizi, ninaomba sasa nirejee katika kuchangia kuhusiana na hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yameongelewa masuala mengi; imegusa masuala ya afya, maji, majanga mbalimbali na imegusa maeneo mbalimbali ikionesha maendeleo makubwa ambayo yamefanywa na Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi kupitia Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza Serikali kwa jitihada ambazo imeendelea kuzifanya katika kuhakikisha kwamba Tanzania inasonga mbele. Tumeyaona maendeleo, tumeona mabadiliko mbalimbali katika sekta mbalimbali na leo ninaomba kuongelea sana katika Sekta ya Afya.

Mheshimiwa Spika, katika Sekta ya Afya Serikali imejitahidi kadri ilivyoweza kwa kuhakikisha kwamba inakarabati Vituo vya Afya, Zahanati, Hospitali za Wilaya, Hospitali za Mikoa lakini pia imeongeza ujenzi wa Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya katika maeneo mbalimbali na hata Hospitali za Mkoa.

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto tu chache ambazo napenda kutoa ushauri wangu ili uweze kufanyiwa kazi. Kujenga Hospitali za Wilaya, Hospitali za Mikoa na Vituo vya Afya ni jambo moja, lakini kuweka wataalam ambao wataenda kuhudumia katika Vituo hivyo vya Afya pamoja na Hospitali ni jambo lingine. Naishauri Serikali sasa, nguvu ambayo iliitumia na kuiwekeza katika ujenzi wa Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na hata Hospitali za Mikoa, nguvu hiyo hiyo ambayo Serikali ilitumia, basi iitumie kuwekeza katika wataalam.

Mheshimiwa Spika, kujenga unaweza kutumia hata mwezi mmoja unapokuwa rasilimali fedha, lakini kuwaandaa wataalam inaweza ikakuchukuwa takribani miaka mitano ili kuwapata wataalam kuweza kutoa huduma za kiafya.

Mheshimiwa Spika, katika huduma za kiafya, tuna- deal na afya za wanadamu. Kwa maana hiyo, ninaishauri sana Serikali sasa iwekeze nguvu katika kuhakikisha kwamba inaandaa wataalam ili waweze kutoa huduma bora za kiafya na siyo bora huduma.

Mheshimiwa Spika, pia waliopo, wale wataalamu tulionao, basi naiomba Serikali itoe kibali ili iweze kutoa ajira katika Sekta hii ya Afya kwa sababu ninaamini kabisa yako maeneo mbalimbali na kwa sababu hapa tunajadili bajeti ya Waziri Mkuu ambayo inagusa maeneo mbalimbali katika nchi ya Tanzania, sitapenda tu nijikite katika mkoa wangu wa mwanza ambao nao pia unahitaji wataalam katika sehemu mbalimbali. Kwa hiyo, ninaomba Serikali iwekeze katika kuandaa wataalam ili waweze kuzihudumia sehemu hizo ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Spika, katika Sekta hiyo hiyo ya Afya kuna suala la hospitali hizi za kikanda, nilikuwa naishauri Serikali iwekeze nguvu kuhakikisha kwamba tunapata hospitali zenye hadhi ya kikanda sawa na Hospitali ya Muhimbili. Tunayo Hospitali ya KCMC ambayo iko Moshi, nashauri kwamba Serikali iweke nguvu ili hospitali hii na yenyewe iweze kuwa na hadhi zawa na Muhimbili ili kuondoa msongamano katika Hospitali ile ya Muhimbili.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuna Hospitali ya Kanda ya Bungando; na yenyewe pia naomba ifanyiwe hivyo hivyo. Pia kuna Hospitali ya Mbeya, Hospitali ya Dodoma General; naomba hospitali hizi ambazo nimezitaja, Serikali iwekeze katika hospitali hizi ili na zenyewe ziweze kutoa huduma sawa sawa na huduma zinazotolewa Muhimbili.

Mheshimiwa Spika, Madaktari bingwa wanaishia kuwepo tu Muhimbili. Ukiwapeleka katika hizo Hospitali ambazo nimekwambia, wanaona kwamba utaalamu wao hauwezi kutumika kwa sababu hospitali zile hazina hadhi sawa na Hospitali ya Muhimbili. Kwa hiyo, ninaomba sana Serikali ijikite katika eneo hilo ili basi tuweze kuboresha huduma za afya katika nchi yetu hii ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, vile vile, katika Vituo vyetu vya Afya na Zahanati zetu tunakosa wataalam wa meno na wataalam wa mionzi. Ninaomba pia Serikali iwekeze katika wataalam hao pamoja na wataalam wengine, lakini ijikite basi katika wataalam wa mionzi na wataalam wa meno ili kuendelea kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa naongelea suala la afya na vile vile katika hotuba ya Waziri Mkuu ameongelea suala la janga hili la Corona, nami naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuwasihi Watanzania kwamba tuweze kuzingatia yale maelekezo ambayo tunapewa na Wizara yetu ya Afya ili tusiweze kueneza ugonjwa huu wa Corona.

Mheshimia Spika, naomba niishauri Serikali na ninaamini kwa ushauri huu wataweza kunisikiliza na kuufanyia kazi. Pamoja na kwamba tumeendelea kutoa maelekezo mbalimbali, lakini ninaangalia sehemu ambazo kuna misongamano mikubwa ya watu, pale kukitokea mlipuko, hali itakuwa ni mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kwenye public transport, ukiangalia pale Dar es Salaam katika haya mabasi ya mwendo kasi, msongamano ambao unakuwepo katika yale mabasi ni mkubwa na ni hatari sana. Ninashauri basi Serikali iangalie namna bora aidha kusitisha hizi public transport hasa ambazo zina msongamano mkubwa na kuangalia njia mbadala ambayo Watanzania wataitumia katika kusafiri kila siku kwenda kufanya majukumu yao mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine yenye msongamano mkubwa ni sehemu ya feri pale Dar es Salaam napo pia kuna msongamano mkubwa. Sehemu kama vile la soko la Kariakoo naomba sana Serikali yangu sikivu iangalie maeneo hayo na iweze kutoa tamko ambalo litaweza likawasaidia watanzania na kusaidia kupunguza spreading hii ya ugonjwa huu wa Corona na hata kuzuia vifo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hiyo naomba sasa niongelee suala la maji,suala la maji limekuwa likipigiwa kelele sana na Wabunge wengi hapa ndani, wakati wa kipindi cha maswali na majibu utaona wakati wa maswali ya nyongeza Wabunge wote husimama kuweza kuulizia masuala ya maji. Lakini pamoja na kwamba Serikali imejitahidi kuchukua mawazo ya Wabunge na kuanzisha wakala wa huduma za maji vijijini yaani RUASA na pia uko mfuko wa maji ambao mfuko huu chanzo chake cha fedha kinatokana na shilingi 50 ya kila lita moja ya petroli.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukiiomba sana Serikali kwamba iongeze kiwango hiki cha tozo ya shilingi 50 hadi shilingi 100 nia ni njema sana. Nitaongea kama ifuatavyo nia na madhumuni tuweze kufikia walau mfuko huu kuwa na shilingi bilioni 300 zikipatikana shilingi bilioni 300 ina maana kila jimbo lina uwezo wa kupata shilingi bilioni 10. Kigugumizi kinatoka wapi, ninaiomba Serikali yangu kwa kuwa ni Serikali sikivu basi iliangalie na hili ili tuweze kumtua mwanamke ndoo kichwani lazima tuongee kwa vitendo na kwa sababu Waheshimiwa Wabunge tumeendelea kutoa ushauri huu wa kuongeza tozo hii ya shilingi 50 hadi 100 ili lengo letu la kufikia shilingi bilioni 300 na hatimaye kila jimbo kupata bilioni 10.Ninaamini kabisa hakuna mtu ambaye atasimama katika Bunge kulalamikia suala la maji, ninaamini kila jimbo litaweza kufanikiwa kuangalia kwamba masuala ya maji yametatuliwa.

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Kiteto.

MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii na naamini kabisa kwamba ushauri ambao nimeutoa Serikali yangu sikivu itaweza kuuchukua nashukuru na naunga mkono hoja ahsante sana.(Makofi)