Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hassan Elias Masala (23 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Naomba kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Nachingwea kwa imani kubwa ambayo wameionesha kwangu ili niweze kuwawakilisha katika Bunge hili Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupoteza muda naomba nijielekeze katika kuchangia Mpango huu, kwanza, kwa kuwapongeza watu wa Wizara wakisaidiwa au wakiongozwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa namna ambavyo wamewasilisha Mpango huu ambao umekuwa na mwelekeo wa kutaka kuisaidia nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa kabla ya yote, nomba niunge mkono wale ambao wametangulia kusema kwamba hatuwezi kutekeleza Mpango huu kama hatuwezi kujielekeza katika kufanya makusanyo mazuri katika kodi, lakini pia katika kupata fedha kutoka vyanzo mbalimbali ambavyo vitatuwezesha kutimiza malengo ambayo tumejiwekea. Mengi yameshasemwa lakini Mipango mingi imeshapangwa kwa kipindi cha nyuma ambacho sisi tumekuwa nje ya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ubunifu wa ukusanyaji wa mapato yetu. Nimeupitia Mpango huu vizuri sana, yako maeneo ambayo nafikiri wenzetu wa Wizara wakisaidiana na wadau mbalimbali wanatakiwa kuendelea sasa kujifunza kutoka katika maeneo mbalimbali ili tuweze kukusanya kodi kwa uhakika tuweze kutimiza malengo ya Mpango wetu. Pia Mheshimiwa Waziri nikuombe tuendelee kutumia wataalam wetu mbalimbali hata walio nje ya Wizara ili waweze nao pia kutoa mawazo ambayo yatasaidia katika kukamilisha Mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo ambayo ningependa nijielekeze kama ambavyo malengo ya Mpango wetu yanavyozungumza. Kuna eneo la viwanda na Serikali ya Awamu ya Tano imejielekeza katika kuimarisha viwanda. Kwa sisi ambao tumetoka Mikoa ya Kusini kwa maana ya Lindi na Mtwara, tumekuwa ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya biashara; tuna korosho, tuna ufuta na sasa hivi tuna mbaazi. Hatuwezi kujadili kujenga uchumi mkubwa wa nchi yetu kama hatuwezi kujadili namna ya kuwaimarisha na kuwaendeleza wananchi katika ngazi ya chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Wilaya ya Nachingwea inavyo viwanda vikubwa viwili ambavyo vimebinafsishwa. Tuna Kiwanda cha Korosho pale Nachingwea na tuna kiwanda cha kukamua mafuta, vyote wamepewa wawekezaji na viwanda hivi vimeshindwa kuendelezwa. Naomba Mheshimiwa Waziri, tunamwomba Rais wetu katika ari hii aliyoanza nayo, hivi viwanda nafikiri kuna kila sababu ya kwenda kuviangalia na tuweze kuvirudisha ili viweze kwanza kutoa ajira kwa wananchi wanaozunguka maeneo yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tuweze kuimarisha upatikanaji wa huduma ili tuweze kuandaa mazao yetu wenyewe katika maeneo haya ya kuanzia ngazi za chini. kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunapojadili viwanda viko viwanda ambavyo tayari hatuhitaji kufanya kazi kubwa ili tuweze kuviendeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulichangia, ni suala zima la miundombinu, Wilaya ya Nachingwea, Mkoa wa Lindi, Mkoa wa Mtwara kwa kutoa hizi malighafi ambazo nimezizungumza ambazo tunahitaji kujenga viwanda bado tumekuwa na changamoto kubwa sana ya mawasiliano na hasa katika eneo la barabara. Leo tunajadili Mkoa kama wa Lindi bado hatujafikia hatua ya kuweza kuunganisha kupata mawasiliano ya uhakika. Bado tuna tatizo la barabara sasa hatuwezi kufikiria kufanya mambo makubwa wakati bado wananchi wetu wanaendelea kupata shida ya usafiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo barabara ambazo toka nimepata akili mpaka leo bado zinazungumzwa na bado hazijafanyiwa kazi. Tuna barabara ya Nanganga - Nachingwea, tuna barabara ya Masasi – Nachingwea, bado tunahitaji barabara hizi zijengwe kwa kiwango cha lami. Pia tunahitaji tujengewe barabara ya kutoka Nachingwea kwenda Liwale na haya ndiyo maeneo ambayo yanazalisha kwa sehemu kubwa mazao ya biashara ambayo nimeyataja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji pia barabara ya kutoka Nachingwea - Ruangwa na barabara zile zinazounganisha Mkoa wa Lindi pamoja na Mkoa wa Mtwara na Mkoa wa Ruvuma. Haya yote ni maeneo ya kiuchumi ambayo kwenye Mpango huu lazima tujielekeze kwenye bajeti yetu tuone maeneo haya yanapata huduma muhimu ili tuweze kufikia malengo ambayo tumejiwekea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa pia kuchangia, ambalo pia nimepitia katika huu Mpango ni eneo la nishati na madini. Tunayo changamoto, naomba niungane na wenzangu kumpongeza Waziri ambaye anashughulika na eneo hili Profesa Muhongo, iko kazi kubwa naomba nikiri kwamba imefanyika na inaendelea kufanyika, lakini bado tunazo changamoto ambazo tungependa kushauri Serikali yetu iongeze jitihada. Leo maeneo mengi ya vijiji vyetu yanapata umeme, lakini tungependa speed iongezwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Muhongo, wananchi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara ndiyo sasa hivi wanatoa gesi ambayo tunaitumia Tanzania nzima. Ni vizuri sasa mipango hii ambayo tunakwenda kuipanga, tuanze kunufaika watu wa maeneo haya ili wananchi wetu waweze kujikwamua na kupata uchumi ambao tunaukusudia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulisemea ni katika upande wa madini. Mkoa wa Lindi na Mtwara bado ziko fursa nyingine ambazo ningependa kuishauri Serikali ijielekeze kufanya utafiti. Sasa hivi Wilaya kwa mfano ya Nachingwea, Mkoa wa Lindi sehemu kubwa ina madini. Madini ambayo bado hayajatumika, madini ambayo bado Serikali haijatambua kwamba yanaweza yakakuza uchumi wa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo madini maeneo ya Nditi, Kilimarondo na Marambo, haya ni maeneo ambayo nimwombe Mheshimiwa Waziri kwa heshima na taadhima, aelekeza wataalam wake waje tutawapa ushirikiano ili waweze kufanya utafiti wa kutosha tuweze kupata madini mengi zaidi ambayo yatalisaidia Taifa letu na pia yatasaidia wananchi wanaozunguka maeneo haya, kwa maana ya kuwapatia ajira na kukuza kipato cha Mtanzania wa kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia ni eneo la elimu. Nimepitia vizuri huu Mpango, naomba niwapongeze kwa kazi kubwa ambayo imefanyika. Naomba nimpongeze kwa upekee kabisa Rais wetu mpendwa aliyepita Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete. Iko kazi kubwa ameifanya ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inatakiwa kuiendeleza. Leo hii nimezunguka ndani ya Jimbo langu Kata zote 32, changamoto kubwa ambayo tunakutana nayo ni ukosefu na upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuliona hili Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alianzisha kwa makusudi jitihada za ujenzi wa maabara. Maabara hizi sasa hivi zimesimama, hazina msukumo; nilifikiri lengo lake lilikuwa ni zuri. Sasa kupitia Mpango huu naomba kwenye bajeti tunayokwenda kuipitisha, maabara hizi sasa tuzitoe mikononi mwa wananchi kwa sababu wamechangia nguvu zao kwa sehemu kubwa, badala yake Serikali ichukue kwa maana iliahidi itatoa vifaa, itamalizia majengo haya ambayo tayari tumeshayajenga ili tuweze kuzungusha tupate Walimu ambao watakwenda kufundisha kwenye shule zetu na tutapata wasomi wazuri wa masomo ya sayansi ambayo watasaidia katika kada nyingi ambazo tumekuwa na tatizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha hili niliona ni pendekezo ambalo nalo pia ningependa kulizungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la afya. Bado kwenye Mpango hatujaeleza ni namna gani Serikali imejipanga kusaidia kuona namna gani tunajenga vyuo vingi zaidi ili tupate wataalam. Leo hii hospitali zetu, zahanati zetu zina matatizo makubwa ya wataalam. Hii tutaipatia majibu kwa kutengeneza mkakati wa kusomesha wasomi wengi zaidi ambao watakwenda kuisaidia nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia, ni eneo hili la uchumi kwa maana ya Mawaziri wetu ambao wamechaguliwa na Mheshimiwa Rais wetu, msaidieni Rais wetu, Rais wetu ameanza vizuri anafanya kazi nzuri. Naomba niwasihi Mawaziri wetu fanyeni kazi, sisi tuko nyuma yenu, tunaahidi kuwapa ushirikiano, lengo letu ni kuwakwamua Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nihitimishe katika eneo la kilimo, naomba nitoe pongezi pia kwa Serikali kwa kazi kubwa inayofanya. Ipo changamoto ambayo nimeiona, ambayo ningependa kuishauri Serikali yangu. Kuna eneo la umwagiliaji, utengenezaji wa miundombinu, pesa nyingi inatengwa kwenda huko, lakini miradi mingi inahujumiwa huko chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba watu wa Kanda, kaka yangu Mwigulu yupo hapa ndani, namwomba afuatilie hili eneo. Pesa nyingi inapotea, miradi mingi ya umwagiliaji haifanyi kazi, nenda Nachingwea, upo mradi mkubwa pale Matekwe ambao ungeweza kunufaisha Watanzania, pesa yote imepotea, hakuna mradi uliokamilika. Nimewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, miradi mingi ya umwagiliaji ni hewa, pesa ukienda inasimamiwa na watu wa Kanda. Naomba Mheshimiwa Waziri fuatilia hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la pembejeo, nimekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Pembejeo, pesa nyingi ya pembejeo Mheshimiwa Waziri inapotea katika eneo hili. Malengo ya Serikali ni mazuri, lakini pesa hii hakuna mtu wa kumwamini sasa hivi. Naomba Serikali kupitia Wizara Fedha, kupitia Wizara ya Kilimo ifuatilie kwa karibu eneo hili. Tulete mapendekezo mazuri yatakayosaidia ili wananchi wetu kweli wanufaike kwa kupata pembejeo kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda, naomba nishukuru, lakini pia naomba niunge mkono hoja juu ya Mapendekezo ya Mpango huu ambao lengo lake ni kuwasaidia Watanzania. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu pembejeo; kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa wa pembejeo kwa wakulima hivyo kuathiri wakulima wetu na kupelekea ufanisi kuwa mdogo katika kilimo cha mazao ya chakula na biashara. Mfano, Wilaya ya Nachingwea, mbegu na mbolea za ruzuku mpaka sasa zipo maofisini, hazijawafikia wakulima kutokana na kuchelewa. Aidha, kumekuwa na utaratibu mbovu wa kuwatumia wafanyabiashara kusambaza pembejeo. Hali hii inapelekea udanganyifu mkubwa kati ya Wasambazaji na Maafisa Kilimo.
(d) Mfumo huu kutokana na kuchelewa kwa malipo unachangia ununuzi holela wa mazao kwa kutumia vipimo visivyo sahihi „KANGOMBA‟
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri ni kwamba malipo yafanyike kwa wakati ili kuwakomboa wakulima, mabenki yabanwe ili kupunguza riba kwa Vyama vya Msingi. Maafisa Ushirika wawe wanabadilishwa vituo mara kwa mara kwa maana waweze kuwa na vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya wakulima kwa kushirikiana na wafanyabiashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya umwagiliaji; miradi mingi ya umwagiliaji haifanyi kazi kutokana na usimamizi mbovu unaofanywa na ofisi za Kanda. Wilayani Nachingwea kuna miradi mikubwa miwili ya umwagiliaji Mitumbati na Matikwe, miradi hii imepewa pesa nyingi lakini haijafikia malengo ya kutoa huduma kwa walengwa kutokana na ubadhirifu na kukosekana kwa usimamizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri ni kwamba, usimamizi wa miradi hii usisimamiwe na ofisi za Kanda, badala yake pesa zielekezwe Halmashauri na zitasimamiwa na Wataalam wetu na Madiwani. Elimu ya mara kwa mara itolewe kwa wakulima juu ya matumizi sahihi ya miradi ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, matumizi ya zana za kisasa; mpaka sasa sehemu kubwa ya wakulima wanatumia zana butu na za kizamani katika kilimo hivyo kuathiri uzalishaji. Hali hii imepelekea uzalishaji mdogo na hivyo kusababisha ukosefu wa chakula na pesa kwa wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Wizara iweke masharti nafuu kwa kushirikiana na makampuni binafsi ili kukopesha matrekta kwa wakulima tofauti na urasimu uliopo sasa. Elimu itolewe kupitia Maafisa Ugani huko vijijini, ajira na semina za mara kwa mara zitolewe kwa Maafisa Ugani na Wakulima wakubwa katika maeneo ya vijijini. Bajeti ya Wizara ielekeze nguvu kwa kununua vyombo vya usafiri mfano, baiskeli, pikipiki magari kwa wataalam wetu ili waweze kusaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mifugo; kumekuwa na migogoro mikubwa kati ya wakulima na wafugaji kutokana na ongezeko kubwa la mifugo na mahitaji ya chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri bajeti ielekezwe katika kufanya mipango bora ya matumizi ya ardhi, hii itaepusha migogoro. Serikali itenge maeneo mapya kwa ajili ya shughuli za wafugaji na wakulima. Elimu ya uvunaji wa mazao ya kilimo na mifugo ifanyike mara kwa mara ili kupunguza idadi kubwa ya mifugo. Kufufuliwa na kuanzishwa kwa ranchi mpya ili kuendeshea ufugaji wa kisasa. Rushwa na vitendo viovu vidhibitiwe dhidi ya wafugaji na wakulima hali hii itapunguza migogoro kwa sababu haki itakuwa imesimamiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kuwa, mfumo wa usambazaji upitiwe upya na pembejeo ziwafikie wakulima mapema. Bei ya pembejeo ipunguzwe ili wakulima waweze kumudu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la stakabadhi ghalani. Kumekuwa na malalamiko mengi kwenye utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi ghalani hivyo kuathiri shughuli za kilimo Jimboni Nachingwea. Kero kubwa ni:-
(a) Kucheleweshwa kwa malipo ya kwanza, ya pili na bonus hivyo kuathiri shughuli za kilimo na kuwaingiza wakulima kwenye umaskini.
(b) Viongozi wa Vyama vya Msingi wakishirikiana na Maafisa Ushirika kuingia mikataba na wafanyabiashara wakubwa kuwaibia wakulima kwa kuwakata makato makubwa wakati wa malipo.
(c) Mabenki kutoza riba kubwa kwa Vyama vya Msingi, hivyo mzigo mkubwa kubebeshwa mkulima.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba ya Wizara ya Elimu.
Mimi naomba nijielekeze kwenye mambo yafuatayo; eneo la kwanza mara baada ya kupitia hotuba nzima nilikuwa anajaribu kuangalia eneo la uboreshaji wa miundombinu katika kuboresha kiwango cha elimu katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa waziri atakapokuja kusimama hapa ni vizuri niungane na wale wenzangu waliotangulia kusema ni kwa kiasi gani wamejipanga kukamilisha ujenzi wa maabara ambao ulishaanza kipindi cha nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivi lengo letu ni kuona tunawezaje kwenda kutatua tatizo la walimu wa sayansi ambalo limekuwa ni tatizo kubwa na hata hapa tunapojadili upungufu wa walimu kwa sehemu kubwa tunaangalia upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna eneo la upungufu wa madarasa na nyumba za walimu naona mkazo mkubwa tumeelekeza zaidi kwenye kujenga madarasa na hii ni kwa sababu ya ongezeko la watoto ambao tumekuwa tumewapokea mara baada ya utekelezaji wa sera hii ya elimu bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni lazima tuangalie mazingira ya walimu wetu, tuone ni namna gani Serikali imejielekeza kujenga nyumba za walimu za kutosha, ukienda kwenye jimbo la Nachingwea ambalo mimi nakaa sehemu kubwa ya walimu wetu hawana makazi ya kudumu yenye kueleweka hivyo hii inaweza ikashusha kiwango cha elimu katika kuboresha elimu yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia Mheshimiwa Waziri Profesa Ndalichako nilifikiri tunapojadili elimu ni lazima tuangalie stahiki za walimu. Walimu wetu wamekuwa kwenye matatizo makubwa ya kudai haki zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wanapandishwa madaraja lakini hawalipwi pesa zao kwa wakati. Nafikiri umesikiliza na umeona kumbukumbu ya idadi ya watu ambao wanadai na kiasi ambacho Serikali kinadaiwa, kwa hiyo naomba deni hili ili tuweze kuwatia nguvu walimu ni lazima tuweke mkakati wa kuona kupitia bajeti hii tunawezaje kwenda kulipa madeni, ili walimu waweze kufanya kazi ambayo tumewaagiza watusaidie kutufanyia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia liko tatizo, iko tofauti ya upandishwaji wa madaraja kwa walimu ambao wameanza wakati mmoja. Walimu mathalani wanaanza mwaka mmoja lakini baada ya miaka mitatu pamoja na kwamba kuna OPRAS ambayo inapima utendaji wao wa kazi lakini bado kumekuwa na variation kubwa katika upandishaji wa madaraja sasa hili ni tatizo na walimu wetu wangependa kupata majibu wakati unahitimisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini kinapelekea utofauti huu mkubwa kwa watu ambao wameanza wakati mmoja kuwa katika viwango tofauti vya madaraja yao na hivyo kupelekea kupokea pesa kidogo tofauti na wale ambao wameanza nao kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuchangia na mimi niungane mkono na wale wote ambao wameshangazwa na maamuzi yale ambayo kimsingi jana Mheshimiwa Waziri ameshayatolea ufafanuzi. Makosa sio wanafunzi, kilichofanywa na TCU lazima Serikali iende zaidi ya pale ambapo imefanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa wako watu wamechukuliwa hatua lakini ni lazima tujiulize tatizo mpaka tumelifuga tunachukua wanafunzi, tunawapa mikopo, lazima tujue tatizo ni kwa nani lazima hatua tungependa kuishauri iende zaidi ya hapo ili kuondoa uzembe ambao kimsingi tusingependa kuona vijana wetu wanapata shida na leo tunakuja kuwabebesha mzigo ambalo wao hawahusiki lakini kumbe kuna watu wamepewa dhamana na wameshindwa kusimamia dhamana yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la mikopo, mim naomba ni-declare interest, Mheshimiwa Waziri kati ya watu unaowatafuta kulipa hiyo mikopo nafikiri na mimi mwenywe ni mmojawapo. Nimeshangaa kidogo hapa lakini nafikiri tuna kazi ya kukusaidia kwamba unatafuta waliokopeshwa wako wapi. Bado unajaribu kuangalia board toka nimeajiriwa Serikalini kabla sijaacha kazi nimejaribu kufanya mawasiliano zaidi ya mara tatu, mara nne niweze kurejesha mikopo lakini sijaona hatua zozote. Sasa hili ni mapungufu ambayo yako ndani ya Bodi ya Mikopo, ni usimamizi mbovu ambao bado haujawekewa mikakati. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, leo hii ukiamua nusu ya Wabunge walioko hapa ndani wote ni wanufaika wa hii mikopo, lakini ni Wabunge wangapi wamelipwa hii mikopo nafikiri hakuna au ni wachache watakaokuwa wamefanya hivi, lakini sio makosa yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ulipaji ule mmeweka gharama za kufidia kile ambacho mmekiita wenyewe kwamba ni sumbufu sijui ni nini. Hebu Mheshimiwa Waziri, tutakaa chini tujaribu kuweka utaratibu mzuri, lengo letu sisi kama Wabunge lazima tuwe mfano tulipe hii pesa ili vijana na watoto wetu waweze kupata na wao elimu kama ambavyo sisi tulipata wakati tunasoma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kukuambia mimi niikuwa Rais wa Serikali ya wanafunzi chuo kikuu pale DUCE mwaka 2008/2009. Najua kinachofanyika Bodi ya Mikopo ni nini, hebu tumia baadhi wa Wabunge wenzio ulikuwa nao hapa ndani tukusaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko account mbili mbili zinafunguliwa na Bodi ya Mikopo, wako watu ambao wanapewa pesa lakini kimsingi pesa hii inarudi kwa watendaji wa bodi ya mikopo wenyewe. Sasa ni jambo ambalo linahitaji utulivu, linahitaji sasa wewe ushirikishe wadau mbalimbali ili tuweze kukupa taarifa ili tuweze kurejesha hizi pesa na vijana wetu waweze kusoma na hata wapiga kura nao waweze kunufaika na mikopo ambayo sisi tumenufaika nayo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulichangia ni suala la ukaguzi wa shule zetu. Leo hii nimeipitia bajeti nzima, najaribu kuangalia kiasi cha pesa ambacho kimeombwa kwa ajili ya matumizi ya kuboresha eneo la ukaguzi wa shule zetu, bado sijaona kiasi cha pesa cha kutosha.
Mheshimiwa Waziri na hili naomba nikwambie itakapofika wakati nitakamata mshahara wako, lazima uniambia ni kwa kiasi gani tumetenga pesa kwa ajili ya Idara hii ya Ukaguzi, leo hii ukaguzi haufanyi kazi yoyote ile, shule zetu hazikaguliwi, miaka mitano, miaka kumi shule zinafundisha, walimu wanafundisha lakini hakuna mtu anayeenda kutoa ushauri ni kwa sababu Idara ya Ukaguzi haina mafuta, Idara ya Ukaguzi hawana magari, Idara ya Ukaguzi hawana vitendea kazi na imefika wakati sasa wanatamani warudishe Halmashauri labda wanaweza kupata msaada kuliko kukaa huko ambako wamekaa na hawapati kiasi chochote cha pesa cha kufanya kazi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, nitaomba wakati unakuja kuhitimisha bajeti yako utuambie watu wa ukaguzi umewatengea kiasi gani cha pesa na sio kiasi cha bilioni mbili ambacho kitaenda kubaki mara baada ya matumizi mengine kwa kadri ulivyoomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la mitaala. Mtaala wetu unaotumiaka na kwa kasi tuliyonayo ya kuhitaji kujenga viwanda bado haiendani. Leo tunahitaji viwanda vya kutosha lakini hatuna wataalam ambao watakwenda kufanya kazi kwenye viwanda vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Elimu ya Kujitegemea (EK) mashuleni haifanyi kazi, leo hii tunategemea tuzalishe wasomi, tuzalishe watu ambao wataenda kuhudumia viwanda vyetu, lakini mitaala yetu inapishana. Leo hii ndani ya nchi moja wako watu wanatumia mitaala ya kutoka kwa Malkia ya Cambridge, kuna Watanzania wanaotumia mitaala ya kawaida sijui tunangeneza taifa la namna gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu tumeamua kujipanga vizuri ni vizuri sasa tukaangalia namna ya kurekebisha mitaala yetu i-match na kile ambacho tunakwenda kukitengeneza ili tuweze kusaidia Taifa hili na Watanzania kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni wakati ule mitaala inapobadilika, vitabu vinavyotumika mashuleni navyo pia haviendani. Leo hii darasa la kwanza na darasa la pili vitabu wanavyovitumia na mitaala ni vitu viwili tofauti. Wachapaji wa vitabu wamekuwa wengi, vitabu hivi vinapishana kimaudhui, vitabu hivi vinapishana katika content ambazo tungetegemea zifundishe watu wa aina moja.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri kwa kazi ambayo umeifanya na unaendelea kuifanya ni vizuri maeneo haya yote tukayaweka vizuri ili tuweze kutengeneza kitu ambacho kinafanana na tutengeneze Watu ambao watakuwa sawa katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingineni ufundishaji wa TEHAMA katika shule zetu. Shule za wenzetu zile ambazo Watoto wenye pesa wanaweza kusomesha leo wanapata masomo ya sayansi, wanasoma computer, wanasoma vitu vingine, lakini ukienda katika shule zetu za kawaida wanapelekewa vitabu lakini practically hawasomi haya masomo kwa ajili ya kuwawezesha na wao kumudu teknolojia hii ya mawasiliano. Kwa hiyo Mheshimiwa katika bajeti yako ni vizuri, nimeona kwamba umetenga kwa jili ya ndugu zetu walemavu lakini bado kwa Watanzania wale walio wengi nao pia ni muhimu ukatueleza eneo hili tumejiweka na tumejipanga vipi ili tuweze kufanya vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo ningependa kuchangia ni NECTA kwenye suala la utoaji wa vyeti vya kuhitimu masomo. Hapa katikati tumeanza na division one mpaka division zero, lakini kuna watu wamekuja kutahiniwa kwa kupewa GPA, kuna watu walikuja wakapewa ile mpaka division five, leo hii waajiri wanapata shida wakati wa kuajiri kujua ni utaratibu gani unaweza ukatumika.
Naomba nitoe ushauri Mheshimiwa Waziri wakati unahitimisha utuambie, Wizara yako inaweza ikaweka utaratibu gani ili vitoke vyeti vya pamoja ambavyo vitasaidia kuondoa hii sintofahamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi kwa Waziri na watendaji wake wote wa Wizara kwa kusimamia na kutekeleza majukumu yao. Wizara ya Elimu ni Wizara kubwa na hivyo ina changamoto nyingi sana ambazo Serikali na wadau wa elimu ni lazima wazitafutie majibu ya uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maboresho katika miundombinu, shule nyingi za kata zimejengwa Tanzania nzima na hivyo kupelekea watoto wengi kupata elimu, lakini shule hizi hazina maabara wala vifaa, nyumba na walimu wa madarasa ni tatizo kubwa hivyo Wizara lazima ijipange kutatua kero hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Wizara kuweka msisitizo kwa elimu ya awali (pre-school) ambako watoto wanakosa uwezo wao kiakili na kupata maarifa mapya. Kwa kuwa maandalizi ya mtaala wa elimu ya awali unaendelea ni muhimu kuangalia vigezo kwa vijana waliohitimu na kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha nne na sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtaala wetu unahitaji kufanyiwa marekebisho ili uendane na dhana ya uwezo (competence based). Kwa sasa elimu yetu japo tunahubiri CBC lakini kinachoendelea mashuleni ni knowledge based. Hakuna uhalisia wa matakwa ya mtaala na kinachofanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iwekeze katika tafiti kwenye taasisi za elimu ya juu kwa maana zimekuwa chache na taasisi hizi zimeacha moja ya jukumu lake ambalo ni ufundishaji, utafiti na ushauri wa kitaalam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la udahili wa wanafunzi wa elimu ya juu liangaliwe upya katika sheria iliyoanzisha TCU na ikiwezekana liachwe kwa vyuo husika, na hii ndiyo practice ya vyuo vingi duniani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tujenge nchi yenye wataalam wa kada mbalimbali ni muhimu Wizara ikapiga marufuku vyuo vya kati kutoa shahada. Vyuo hivi vitoe astashahada na stashahada. Kwa sasa nchi inakosa wafanyakazi wa kawaida kwa maana wenye shahada hawawezi kufanya kazi ambazo zinaweza kufanywa na watu wa kata, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko Mezani. Kabla ya kuendelea mbele naomba nijumuike na wenzangu waliotangulia kutoa shukrani lakini pia kutoa neno la pongezi kwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Magufuli kwa kazi kubwa na kazi nzuri ambayo imekuwa inafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri wote wa Wizara zote mbili kwa uwasilishaji mzuri na yale waliyoyawasilisha ambayo leo hii tunayajadili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie maeneo makubwa yasiyopungua matano lakini nitajielekeza zaidi katika Jimbo ambalo natokea la Nachingwea, lakini wakati huo huo tutakwenda kuangalia namna gani ambavyo yana-reflect Taifa kwa ujumla katika kuhakikisha tunasonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ambalo napenda kuchangia ni elimu. Katika Jimbo la Nachingwea na kwa ukongwe wa Wilaya ya Nachingwea tuna kazi kubwa ambayo tunatakiwa tuendelee kuifanya pamoja na jitihada ambazo Serikali imeendelea kuzifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwenye suala la elimu bure ambayo imeanza kutolewa mwaka huu ni jambo ambalo limepokelewa vizuri sana na wananchi wa Jimbo langu la Nachingwea. Nimefanya ziara katika kata zangu zote 34, maeneo yote niliyopita takwimu za uandikishaji zimekwenda juu, hii tafsiri yake ni nini? Kwa mwananchi wa kawaida ambaye alishindwa kupeleka mtoto wake shule sasa hivi jambo hili limepokelewa kwa namna ambayo kwetu sisi wanyonge limekuwa ni jambo la kheri. Kwa hiyo, lazima tuipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi hii ambayo imeamua kuifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kupokelewa kwa elimu bure, yako maeneo ambayo nimeona kuna changamoto ambazo ningependa kuishauri Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni kuangalia namna gani tunaweza tukaongeza bajeti ili tuweze kukabiliana na hizi changamoto ambazo tumeanza kuziona katika kipindi hiki cha mwanzo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo sasa hivi watoto wanakaa chini kama ambavyo tumezungumza, hii ni kutokana na ukosefu wa madawati lakini pia yako maeneo ndani ya Jimbo la Nachingwea watoto wanasomea nje kwa maana hawana madarasa. Kwa hiyo, naomba niungane mkono na wale wote waliotangulia kuomba Wizara ya TAMISEMI ijielekeze kwenye kuongeza bajeti ili tuweze kupata majengo ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba wananchi wanaendelea kutu-support kufyatua tofali na kujitolea wao wenyewe kujenga miundombinu hii, lakini ni muhimu pia Serikali ikaona umuhimu wa kuongeza jitihada ili tuweze kupata pesa hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuishauri Serikali ni eneo ambalo linahusiana na uendeshaji wa mitihani. Nimefanya mazungumzo na walimu katika shule zote za ndani ya Jimbo langu. Moja ya changamoto kubwa ambayo naiona ni lazima tuiwahi, ni eneo la ukosefu wa pesa za uendeshaji wa mitihani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mitihani hii kwa kipindi cha nyuma kwa sehemu kubwa ilikuwa inategemea michango ya wazazi, sasa hivi baada ya kuondolewa, tayari pesa inayopelekwa kwa idadi ya wanafunzi katika shule, haiwezi kutosheleza kuendesha mitihani mitatu mpaka minne kwa mwaka. Na mimi kama mwalimu natambua umuhimu wa kutoa mazoezi kwa watoto. Usipotoa mazoezi kwa watoto, watakwenda kufanya mitihani vibaya.
Kwa hiyo, ni lazima tujielekeze kutenga pesa ya ziada ambayo itaelekezwa katika kutoa huduma hii ya mitihani ili kuwapima watoto wetu waweze kufanya vizuri katika mitihani yao ya mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine katika upande wa elimu ni ujenzi wa maabara. Ujenzi wa maabara umefanyika Tanzania nzima. Kwa Jimbo la Nachingwea, ndani ya kata 29 tayari wananchi walishapokea wito wa kujenga maabara. Maabara hizi zitatupelekea kupata walimu wa masomo ya sayansi; na hili ndilo tatizo kubwa sasa hivi tulilonalo Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Jimbo la Nachingwea walimu wa masomo ya sanaa siyo tatizo, sasa hivi tatizo ni walimu wa masomo ya sayansi. Ili tupate walimu wa masomo ya sayansi ni lazima tukamilishe ujenzi wa hizi maabara ambazo zimejengwa.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Simbachawene, una kazi ya kufanya sasa kaka yangu ili tuweze kupambana. Pale wananchi walipofanya na wameshamaliza nguvu zao, sasa ni muhimu na sisi tukaelekeza pesa ambayo itaenda kumalizia ujenzi wa haya majengo, lakini pia tupate vifaa ambavyo tutakwenda kufundisha watoto wetu kwa vitendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili liende sambaba na suala zima la uboreshaji wa stahiki za walimu. Walimu wetu wanafanya kazi katika mazingira magumu. Tunahitaji kulipa madeni yao yote ambayo wanatudai. Nakubaliana kwamba madeni hayawezikuisha kwa sababu kila siku walimu wanaajiriwa na hii ni sekta kubwa ambayo imebeba watumishi wengi, lakini ni muhimu tukahakikisha tunalipa madeni ya walimu wetu kwa wakati ili waweze kufanya kazi na waende sambamba na hili suala la utoaji elimu bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo napenda kulichangia ni suala la maji. Nachingwea kuna tatizo la maji. Nachingwea ni Wilaya kubwa kama ambavyo nimesema, lakini pia nachukua nafasi hii kumpongeza Naibu Waziri wa Maji, Mzee wangu Mheshimiwa Kamwelwe; alifika Jimbo la Nachingwea akajionea hali halisi ya pale. Ipo miradi ya World Bank ambayo inatekelezwa ndani ya Jimbo la Nachingwea, lakini bahati mbaya tulishamwambia, miradi saba iliyopo ndani ya Jimbo la Nachingwea haifanyi kazi mpaka sasa hivi, pamoja na kwamba pesa nyingi imetumika kujenga miradi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mzee Kamwelwe, lakini pia naomba niseme Mheshimiwa Waziri wa Maji, ambaye nafikiri atakuwa ananisikia, wananchi wa Nachingwea bado kuna ahadi walipewa na wanasubiri majibu juu ya miradi hii ambayo nimeisema ambapo inaonekana kuna uzembe wa baadhi ya watendaji wameamua kutumia pesa kinyume na utaratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara hizi, jibu linasubiriwa na wananchi wa Nachingwea, na mimi nimetumwa, naomba niliwasilishe mbele yenu ili tuweze kusaidiana kulifanyia kazi, tuhakikishe tunachukua hatua pale ambapo mambo hayajaenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine katika upande wa maji, ni ukamilishaji wa mradi wa maji ya Mbwinji ambayo unatoka Masasi, lakini inagusa Vijiji vya Nachingwea na Vijiji vya Ruangwa ambako anatoka Mheshimiwa Waziri Mkuu. Hali ya maji katika baadhi ya maeneo ndani ya maeneo yanayopita mradi wa Mbwinji siyo nzuri. Kwa hiyo, naomba nikumbushe Serikali yetu, katika bajeti hii tunayoenda kuipitisha, ni lazima miradi hii twende tuifanyie kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo napenda kulizungumzia; na hili nitoe ushauri; ni miradi ya TASAF. Naomba niungane na Watanzania wote kuthamini na kutambua kazi kubwa ambayo inafanyika katika kutekeleza miradi ya TASAF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo ambayo nimeona kuna upungufu. Wakati pesa za kutoa kwenye kaya masikini zinatolewa, kuna ushauri tuliutoa, lakini haukupokelewa. Sasa hivi naona kuna umuhimu Serikali hii ya Awamu ya Tano ifikirie namna ya kuboresha eneo hili. Pesa hii kuwapa wale wananchi mkononi kama ambavyo inafanyika sasa hivi, haina tija. Nimezunguka katika vijiji vyangu, nimefanya tathmini kuona ni kwa namna gani wananchi wananufaika na hizi pesa, bado sijaona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Mheshimiwa dada yangu Angellah, kama tunaweza kubadilisha mfumo, ni vizuri pesa hizi sasa hivi na hasa kwa wananchi wa Jimbo la Nachingwea, tukawanunulia matrekta badala ya kuwapa pesa. Matrekta haya yatawasaidia wao wenyewe katika vijiji vyao, kwa sababu kutibulisha ekari moja shilingi 50,000; wanaweza wakatibulisha kwa shilingi 20,000 au shilingi 30,000 tukapunguza gharama. Baada ya kufanya hivyo, nafikiri tunaweza tukaona tija ya pesa hii badala ya kuwapa pesa mkononi ambayo mwisho wa siku wanatumia kutafuta chakula na bado wanaendelea na umasikini wao. Kwa hiyo, hili niliona nilitoe kama ushauri. Eneo hili pia naomba liendane na ile shilingi milioni 50 ambayo inaenda kutolewa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 50 hii lazima tuwe makini, nayo pia tuwe makini; nayo tungeiratibu, siyo kwa kwenda kutoa katika vikundi kama ambavyo imeshauriwa. Hii bado nilikuwa naona vijiji vipewe maelekezo ya namna gani vinaweza vikabuni miradi ambayo itaenda kunufaisha kijiji na ikasimamiwa na kijiji, badala ya kuwapa pesa ambazo tuna hakika zinakwenda kupotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vikundi vingi sasa hivi vinafufuliwa kwa sababu kuna hii pesa. Baada ya hii pesa kutolewa nina hakika vikundi hivi vitakufa na vitapotea kitu ambacho sioni kama tutakuwa tumeisaidia nchi yetu na Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia, ni afya. Zipo changamoto ambazo tunaziona lakini bado tunahitaji kuendelea kuiunga mkono Serikali yetu. Kuna eneo la CHF…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nigusie maeneo manne yale yanayogusa Jimbo la Nachingwea ambalo natokea, lakini yapo ambayo yatagusia ukanda mzima wa kusini mwa Tanzania na yale yanayohusu Taifa letu kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi kwa hotuba nzuri nimeipitia hotuba yake vizuri sana, naomba nimpe hongera kwa kazi nzuri na tunamtakia kila la kheri katika kutimiza ahadi ya yale yote ambayo yamezungumzwa hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya salamu hizo na pongezi hizo naomba sasa nijielekeze kwenye hoja zinazohusu barabara zetu. Uchumi wetu kwa sehemu kubwa unategemea barabara ambazo lazima ziwe katika kiwango cha lami ili tuweze kuleta maendeleo ambayo tunayakusudia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi kwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano lakini pia kwa Serikali ya Awamu ya Nne. Serikali ya Awamu ya Nne imefanya kazi kubwa, mimi natoka mkoa wa Lindi na wale wanaotoka mkoa wa Mtwara watakubaliana na mimi. Miaka kumi iliyopita tulikuwa tunatumia zaidi ya wiki moja kuifikia Dar es Salaam, lakini sasa hivi tunatumia saa nne au tano; unatumia gari ndogo hata taxi kufika Mtwara na Lindi. Hii yote ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa ambayo kwanza ilianza kufanywa wakati wa Mheshimiwa Magufuli akiwa Waziri na sasa hivi ndiye Rais wetu, kwa hiyo, hatunabudi tumshukuru na tumpongeze kwa kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo baadhi ya Wabunge hapa wanachangia mimi nashangaa na nitashangaa sana, kupitia bajeti hii mtu anasimama hapa anasema tunapewa vihela vidogo hivi wakati kuna maeneo ambako wanatafuta pesa hizo waweze kujengewa miundombinu waweze kupata huduma. (Makofi)
Mimi nafikiri ifike wakati sasa tunapokwenda kutekeleza bajeti hii baadhi ya maeneo ambayo hawaoni umuhimu wa hizi kazi tunazozifanya hebu tuachane nao tuelekeze nguvu zetu sasa kwenye yale maeneo ambayo Watanzania wanahitaji kuona miundombinu bora na wanahitaji kuboresha huduma zao badala ya kukaa na kuja hapa kusema maneno ambayo kimsingi hayana mbele wala nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba sasa nirudi kwenye barabara ambayo kwa muda mrefu imekuwa inazungumzwa. Mheshimiwa Waziri Mbarawa nafikiri unakumbuka ulikuja Nachingwea mwaka jana kama sio mwanzoni mwa mwaka huu, umeona hali ya barabara ya kutoka Nachingwea kwenda Masasi na kutoka Nanganga kwenda Nachingwea. Nashukuru kupitia bajeti hii imeorodheshwa na imesemwa kwa kilometa 91; zipo kazi ambazo wakati unakuja kuhitimisha ningeomba unipe ufafanuzi kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nachingwea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumza kwamba maandalizi yanafanyika kwa ajili ya barabara hii, sasa sijajua maana kama ni feasibility study tayari kazi hii imeshakamilika kwa mujibu wa taarifa nilizonazo. Hapa nimeangalia imetengwa shilingi bilioni moja, sijajua hii shilingi bilioni moja ni kwa ajili ya nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana ndani ya mkoa wetu wa Lindi leo tunajadili shughuli za kiuchumi, kwenda kuweka viwanda kwa ajili ya mihogo, kuona namna gani tunaboresha mazao yetu ya korosho na ufuta lakini bado hatujawa na miundombinu ya uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pamoja na kazi nzuri ambayo imefanyika na Serikali yetu bado nimuombe Mheshimiwa Waziri atakaposimama awaeleze wananchi wa Jimbo la Nachingwea ambao wanapakana na wananchi wa Jimbo la Ruangwa, Masasi na Liwale; lazima haya maeneo yote tuelezwe katika bajeti hii Serikali imejipanga vipi kuhakikisha tunajenga hizi barabara kwa kiwango cha lami badala ya kufanya periodical maintenance ambayo kila wakati tunalazimika kuingia gharama kubwa na barabara hizi bado zinakuwa zinaleta usumbufu mkubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni lile ambalo linagusa barabara zinazounganisha mkoa wetu wa Lindi. Tunayo barabara inayotoka Nanganga kwenda Nachingwea. Barabara hii ikijengwa kwa kiwango cha lami inaenda kuunganika na mkoa wa Ruvuma kupitia njia ya Kilimarondo. Kwa muda mrefu barabara hii imekuwa ni muhimu sana kiuchumi katika maeneo yetu.
Kwa hiyo, ningeomba kupitia Wizara Mheshimiwa Waziri tuione barabara hii ili tuiweke katika mipango yetu tuweze kujenga kwa kiwango cha lami tuunganishe na mkoa wa Ruvuma ili tuweze kuunganika na mkoa wa Mtwara na tufungue maendeleo ya mikoa ya Lindi Mtwara pamoja na Ruvuma ambayo kwa muda mrefu kidogo tumekuwa nyuma katika shughuli za maendeleo. (Makofi)
Mheshimwia Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumza nje ya barabara ni eneo la viwanja vya ndege. Wapo baadhi wamezungumza kutoona umuhimu wa viwanja vya ndege. Mimi naomba niseme viwanja vya ndege ni muhimu, kwa nchi yetu hapa ilipofikia inahitaji kujenga viwanja katika maeneo yake. Hapa katika orodha ya viwanja ambavyo vitakarabatiwa kipo kiwanja cha Lindi kimetajwa hapa, kiwanja hicho kina hali ngumu
sana kwa sisi watu wa Mkowa wa Lindi. Lakini kwa Nachingwea, leo viongozi wote wanatua Nachingwea ndipo wanakwenda katika maeneo mengine. Kwa muda mrefu Mheshimiwa Benjemini Mkapa ametumia uwanja wa Jimbo la Nachingwea kwenda Masasi, na sasa hivi hata Waziri Mkuu anapokwenda Ruangwa lazima atue Nachingwea; na bado mahitaji ya watu wa Nachingwea kuweza kutumia ndege na viwanja vyake bado ni makubwa sana. Kwa hiyo wakati Mheshimiwa Waziri anakiangalia kiwanja cha Lindi bado kiwanja cha Nachingwea tungependa kuona hata ukarabati unafanyika kwa sababu ndicho kiwanja kikubwa ndani ya mkoa wa Lindi ambacho kinaweza kikaruhusu kutua kwa ndege na kuweza kufanya safari kuelekea maeneo ya pembezoni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni eneo la mawasiliano ya simu. Naomba nipongeze Wizara, ipo kazi kubwa imefanyika lakini pia kupitia kitabu ambacho ninacho hapa Mheshimiwa Waziri naomba nikupongeze. Ninazo Tarafa za Kilimarondo, Ruponda kule kwangu Nachingwea. Tarafa hizi kwa sehemu kubwa zimeshapata mitandao ya simu na hasa mtandao wa TTCL, hata katika orodha ya vijiji na Kata ambazo zina maeneo haya mmeorodhesha. Lakini bado mtandao wa TTCL kwa wananchi au wakazi wa haya maeneo ambayo nimekutajia Mheshimiwa Waziri bado hawajapata mawasiliano ya uhakika zaidi, wanashindwa kupata huduma za fedha kwa sababu TTCL hawajaingia katika biashara hiyo. Kwa hiyo, tungeomba mitandao kama ya Vodacom, Airtel; na orodha hii tayari tumeshaleta Wizarani, tungependa katika awamu hii uweze kutoa msukumo ili tuweze kupeleka mawasiliano wananchi wale waweze kuunganika na watu wengine wa maeneo mengine ya Wilaya ya Nachingwea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na waliotangulia kusema juu ya suala la uuzaji wa nyumba za Serikali. Mimi ni miongoni mwa Wabunge ambao siungi mkono utaratibu ambao ulitumika kuuza nyumba za Serikali. Utaratibu ule hauna tija kwa Taifa letu. Leo hii viongozi wanateuliwa, Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa, baadhi ya Mawaziri wanakwenda kukaa katika nyumba za wageni badala ya kwenda kukaa kwenye nyumba za Serikali. Hii ni hasara kwa Taifa letu na haya maamuzi kimsingi bado hatujachelewa, kupitia Serikali ya Awamu ya Tano naomba niishauri Serikali yangu, kwa heshima na taadhima hebu ifanye maamuzi ambayo ni magumu ya kurejesha nyumba zote ambazo ziliuzwa bila utaratibu ili watumishi wetu waweze kuzitumia na tuweze kuona namna bora ya kuweza kuboresha watumishi wetu na watu wa kada mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kwa ufupi ATC. Naomba nipongeze jitihada ambazo Mheshimwia Waziri amezizungumza za ununuzi wa ndege japo ni ndege chache, tumechelewa na kimsingi tunapaswa tukimbie sasa kwa sababu idadi ya ndege tulizonazo ni chache na ni aibu kwa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaunga mkono bajeti hii lakini tunaomba watu wa Wizara wawe active waweze kuona wenzetu ambao wameendelea kwenye nchi mbalimbali ukienda kama Dubai - Emirates kule, ukiangalia katika maeneo ya Qatar, wana ndege nyingi, walitumia njia gani? Sisi tunao wasomi ambao wanaweza wakaishauri Serikali yetu na Wizara wakaona namna ya kuweza kuongeza idadi ya ndege kutoka hizi mbili ambazo leo tunazizungumza na tukawa na ndege nyingi ambazo zinaweza zikatua katika maeneo mengi ndani na nje ya nchi yetu. Kwa kufanya hivyo nafikiri tutakuwa tunatafsiri kwa vitendo uchumi ambao tunauzungumza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe kwa kuzungumzia reli ya Mtwara, Mbamba Bay pamoja na…
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafsi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu pamoja na Serikali yake kwa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Mafanikio makubwa yameonekana ndani ya mwaka mmoja ambao tunakwenda kujadili bajeti ya Awamu ya Pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kutoa mchango wangu katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni kilimo, kama ambavyo limezungumziwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nataka nijielekeze katika kilimo cha zao la korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, yako baadhi ya mapendekezo ambayo nilitaka niyatoe ili kuweza kuboresha Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Kwanza tunaipongeza Serikali, mwaka 2016 tulileta hoja hapa za kuondoa tozo ambazo zilikuwa ni kikwazo kwa wakulima wetu. Takriban
tozo tano ziliondolewa na hii ilipelekea kuweza kupata bei kubwa mpaka kufikia 3,800 kwa zao la korosho. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nachingwea na wananchi wa Kusini kwa ujumla, tunaomba tuseme ahsante kwa Serikali yetu sikivu kwa kufuatiliwa kilio chao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, mambo ambayo nilitaka niboreshe kwanza ni eneo la ucheleweshaji wa malipo. Minada imekuwa inafanyika na kwa mujibu wa catalogue za ufanyikaji wa minada, minada ile ilikuwa inatakiwa malipo yafanyike ndani ya siku zisizopungua sita, lakini kwa bahati mbaya makampuni mengi ambayo yalikuwa yanashinda zabuni ya kuchukua korosho za wakulima walikuwa wanachelewesha malipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka leo ninapozungumza, toka mwezi wa Kumi na Moja kuna baadhi ya wakulima ndani ya eneo langu na maeneo ya Kusini baadhi, bado hawajapata malipo yao. Kwa hiyo, hii ni sehemu ya kero ambayo nafikiri Wizara pamoja na wadau wote wa zao la korosho lazima tujitahidi kurekebisha kasoro hizi ili mfumo uweze kuwa mzuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo napenda kushauri ni suala zima la usajili wa vyama, hasa Vyama Vikuu wa Ushirika. Kwa Jimbo langu la Nachingwea tunatumia Chama Kikuu cha Lunali. Chama hiki kinajumuisha Ruangwa, Nachingwea pamoja na Liwale. Naomba tayari wameshaanza kuonesha utashi wa kwenda kusajili mara baada ya kukamilisha taratibu za kufilisi Chama Kikuu cha IIulu ambacho kilikuwa kinahudumia wakulima wa Mkoa wa Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kupitia bajeti tunayoenda kuijadili, jambo hili litiliwe mkazo, sisi tunaotumia chama ambapo sasa hivi ni Kamati ya muda, tuweze kupata chama kikuu ambacho kitaenda kusimamia maslahi ya wakulima wa zao la korosho kabla hatujaingia
katika msimu wa korosho ndani ya mwezi wa Kumi kuanzia mwaka huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ambalo nataka nishauri pia katika kilimo ni eneo la ajira kwa Watendaji. Kwa kipindi cha nyuma, kabla ya mfumo haujaboreshwa, Watendaji wengi ambao walikuwa wamechukuliwa katika Vyama vya Ushirika ni wale ambao hawakuwa na uwezo
lakini pia hawakuwa na elimu ya utunzaji wa fedha.
Mzunguko wa fedha katika msimu wa mwaka huu, umefikia siyo chini ya shilingi bilioni 40 katika Mkoa wa Lindi. Ukiangalia Watendaji ambao wanatoa fedha kwa wakulima, uwezo wao ni mdogo sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa sababu mapato yamekua na fedha imeongezeka, naomba niishauri Wizara ya Kilimo itoe maelekezo kwa Vyama vyote Vikuu vya Ushirika na Vyama vya Msingi vitoe ajira kwa watu ambao wana elimu ya utunzaji wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii nina vyama vitatu ndani ya Jimbo langu, wahasibu wake wana kesi, wamepelekwa Mahakamani kwa sababu ya kupoteza fedha za wakulima na hii yote ni kwa sababu walishindwa kutoa fedha kwa taratibu za kifedha jinsi inavyotaka. Kwa hiyo, ili
tuweze kuwasaidia vizuri, ni lazima ajira sasa za wale Wahasibu wa hivi vyama zitolewe kwa watu ambao angalau wana elimu ambayo itaweza kuwasaidia kuweza kutunza fedha za wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilitaka nishauri katika kilimo ni suala la usimamizi wa tozo ambazo zimeondolewa. Ziko tozo katika zile tozo tano, bado mwaka huu, katika msimu huu zimeendelea kufanya kazi. Kwa mfano, iko tozo ya usafiri iliondolewa na hii tozo iliondolewa kwa sababu tulishauri maghala yatakayotumika, yatumike yale ambayo yako katika ngazi ya Vijiji pamoja na Kata. Bahati mbaya kutokana na kuchelewa kuanza kwa msimu, maghala yaliyotumika ni maghala makuu tu. Kwa hiyo, tozo ya usafiri ikalazimika kurudi tena na hivyo kuwakata wakulima kinyume na makubaliano na sheria ambayo tayari tulishaipitisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo naomba hili tulichukue, safari hii tungependa kuona maghala yote katika ngazi ya Kata, Vijiji yanakarabatiwa mapema iwezekavyo ili tozo hii ambayo ilijirudia, isijirudie tena katika msimu huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho katika kilimo ni suala zima la pembejeo za ruzuku. Mwaka 2016 kwa maana ya msimu huu wa kilimo, Mkoa wa Lindi peke yake tumepokea tani 80. Themanini ukigawanya katika wilaya sita maana yake ni takriban kila wilaya ilikuwa inaenda kupata tani zisizopungua 20 mpaka 18, kitu ambacho ilikuwa ni utani mkubwa sana. Sasa hili naomba watu wa Wizara waliangalie; tunataka kilimo, tunataka tuimarishe viwanda; unapoleta mbegu tani 80 kwa mkoa mzima, ukagawanywe kwa wilaya sita, kwa kweli hii imetushangaza sana, hatujajua tatizo ni nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba watakapokwenda kujumuisha, watuambie kwa nini Mkoa wa Lindi safari hii tani za mbolea na mbegu za ruzuku ambazo mpaka sasa hivi ninavyozungumza zimeshindwa kwenda kwa wakulima, hazijaletwa kwa wingi kama ilivyo mikoa mingine
ukilinganisha na Iringa na Mbeya ambako wamepeleka ziadi ya tani 1,000 wakati Mkoa wa Lindi na Mtwara, jumla yake tani hata 200 hazifiki? Hili tunaomba tupate ufafanuzi ili tujue kama Mkoa wa Lindi na Mtwara kwa sasa hivi hatushiriki kilimo au kuna jambo gani ambalo linaenda kujitokeza?
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo napenda kuchangia katika hotuba ya Waziri Mkuu ni eneo la maji. Naipongeza Wizara ya Maji, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake; walikuja Jimboni kwetu Nachingwea wameona hali halisi. Tunao mradi
mkubwa wa maji ya Mbwinji pale Nachingwea sasa hivi, unafanya kazi nzuri. Moja ya ahadi ambayo ilitolewa ni kuhakikisha maji yanasambazwa umbali wa kilomita tano katika vijiji vinavyozunguka yale maeneo ya chanzo kikuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti hii tunayoenda kuimalizia, jumla ya shilingi bilioni moja ilitengwa. Shilingi bilioni moja hii ilitakiwa itumike kwa watu wa Masasi, Nachingwea pamoja na Ruangwa. Ndani na Wilaya ya Nachingwea tumepata vijiji sita; tuna kijiji cha Naipanga,
Mtepeche, Mkotokuyana, Mandai pamoja na Chemchem. Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipate ufafanuzi wakati unapokwenda kujumuisha kiasi hiki cha fedha ambacho tayari mchakato wa kumpata mkandarasi umeshafanyika, ni lini sasa mradi huu unaenda kutekelezwa ili wananchi wa haya maeneo niliyoyataja waweze kupata maji safi na maji salama ili tuweze kuwasaidia wananchi
wetu ambao kwa kweli wanateseka kwa adha ya kupata maji umbali mrefu?
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ambalo napenda kuchangia katika hotuba hii ni suala la barabara. Mheshimiwa Rais alipofika Nachingwea, alitoa ahadi ya kusimamia, kuhakikisha ujenzi wa barabara ya Nachingwea - Masasi, Nachingwea - Nanganga inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 niliposimama hapa kuuliza swali, niliomba kupata ufafanuzi kwa sababu feasibility study ilishakamilika, ni lini barabara hii itajengwa? Bahati mbaya tulipata shilingi bilioni moja; naomba kupitia bajeti hii ambayo tunaijadili, nijue kupitia utaratibu wa watu wa Wizara ya Ujenzi, wana mkakati gani sasa wa kwenda kuhakikisha barabara hii ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, lakini tayari imeshakidhi vigezo ni lini itaaanza kujengwa kwa kiwango cha lami ili tuweze kuunganisha kati ya Wilaya za Nachingwea, Ruangwa, Liwale pamoja na Masasi ambao ni Mkoa wa Mtwara?
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri Mheshimiwa Waziri Mkuu anajua namna gani ambavyo tunahangaika kupata adha kubwa ya usafiri katika maeneo haya yote. Kwa hiyo, watu wa Wizara ya Ujenzi, tunaomba sana watu wa mikoa hii na maeneo haya waweze kuangalia kilio chetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni la nishati. Mkoa wa Lindi na Mtwara kwa sasa tuko gizani. Hali ya upatikanaji wa umeme siyo ya uhakika. Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimshukuru
Mheshimiwa Waziri, amekuwa akitolea majibu mazuri pale tulipomwuliza, lakini naomba pamoja na kujenga kituo kile ambacho kiko pale maeneo ya Mnazi Mmoja, bado naomba nijue ni jitihada gani ambazo Wizara inakwenda kufanya, kwa sababu sasa hivi mashine zinazofanya kazi kwa umeme ambao unasambazwa mikoa yote miwili, hazizidi mashine nne. Je, tukishajenga kituo tunachojenga, bado inaweza kwenda kuwa ni suluhu ya kudumu ukiondoa jitihada nyingine za kuongeza mashine?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia Wizara, naomba Mheshimiwa Muhongo Profesa wangu, tusaidie watu wa Mikoa hii ya Lindi na Mtwara. Kuna utaratibu gani kupitia Wizara za kuongeza hizi mashine ambazo zitakwenda kututoa gizani sasa hivi kama ambavyo hali imekuwa? Pia naomba na nitafurahi sana nikimwona anakuja katika maeneo haya ambayo sisi kwa muda mrefu wananchi wetu wametutupia lawama kwamba hatusemi na hatujawasilisha kero hii ambayo kwa kweli imekuwa ni changamoto kwa maendeleo ya Wilaya kubwa kama ya Nachingwea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri tukishamaliza kikao hiki atutembelee katika haya maeneo ili kuona hali halisi ya namna tunavyopata athari.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ambalo nataka nilizungumzie ni suala la ajira kwa vijana. Nampongeza Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana pamoja na Naibu Waziri, rafiki yangu, Ndugu yangu, Mheshimiwa Anthony Mavunde, wamekuwa wanafanya kazi, ni wabunifu
wa project mbalimbali ambazo zinaenda kuwainua vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie katika eneo moja, sisi Lindi na Mtwara tuna vyuo hivyo ambavyo tumevitja. Tuna VETA Lindi na Mtwara. Programu ambazo zimepitishwa… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana lakini pia niungane na wenzangu kutoa pongezi kwako pamoja na Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha bajeti kuu ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo imani kubwa sana na utendaji wa kazi ambao unafanywa na Serikali yetu ya Awamu ya Tano, hivyo mambo mengi ambayo yamewasilisha katika bajeti yetu hii nimekuwa na imani nayo kubwa sana juu ya utekelezaji wake na hii ni kwa sababu yako mambo yaliahidiwa mwaka jana wakati wa kampeni na mwaka huu tumeshuhudia tayari yameshaanza kutekelezwa. Kwa hiyo, nitajielekeza zaidi kwenye kushauri yale mambo ya msingi ambayo lengo likae katika kuboresha ili Serikali yetu iweze kutoa huduma kwa wananchi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kila Mbunge aliyesimama hapa katika Bunge hili amesimama kuzungumzia changamoto zilizoko katika majimbo yetu. Wengi tumezungumzia masuala ya maji, barabara, viwanda, lakini pia tumezungumzia suala la uboreshaji wa huduma. Hizi huduma zote hatuwezi kuzileta na Serikali yetu haiwezi kufanikiwa kama haiwezi kukusanya kodi, Serikali yetu lazima ikusanye kodi na hizi kodi zinakusanywa katika vyanzo mbalimbali. Sasa nimuunge mkono Mheshimiwa Waziri wetu kwa yale aliyotuletea ambayo yanaakisi na yana lengo la kutaka kuonesha namna gani ambavyo tumedhamiria kwenda kuwaletea wananchi wetu maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo ninaunga mkono kwanza katika eneo la kukata kodi kwa Wabunge, jambo hili lazima tulipe nguvu na sisi lazima tuwe mfano hata kama limekuja kwa wakati huu nafikiri katika hitimisho Mheshimiwa Waziri atakwenda kufafanua zaidi kwa nini amelileta kwenye bajeti hii wakati anajua suala hili la posho za Wabunge kwa maana ya kile kiinua mgongo kinaenda kupatikana ndani ya miaka mitano au minne ijayo.
Kwa hiyo, mimi ninaunga mkono katika hili na tutakuwa wa kwanza katika kuhakikisha Serikali yetu inatimiza malengo yake ya kuwatumikia wananchi kama ambavyo wafanyakazi wengine, wananchi wa kawaida na wao tunavyowahimiza kulipa kodi na sisi lazima tuonyeshe mfano katika hilo eneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ningependa nalo pia kulizungumzia ni eneo la ukataji wa tozo katika mazao ya biashara ahadi hii ilitolewa na Mheshimiwa Rais wakati anafanya kampeni, aliahidi mara atakapoingia madarakani ataondoa kodi au tozo zote ambazo ni kero. Kwa sisi watu wa Mikoa ya Kusini tunapongeza na naomba nitoe salamu za wananchi wa Jimbo la Nachingwea, wananchi wa Jimbo la Ruangwa jirani zetu pale kwa sababu ni wadau wakubwa wa zao la korosho wamefurahishwa sana na kitendo cha Serikali kuondoa tozo hizi tano ambazo zilikuwa ni tatizo na kwa kiasi kikubwa ziliwarudisha nyuma wakulima wa Mikoa ya Lindi na Mtwara.
Kwa hiyo, sisi tunaunga mkono muhimu na ambacho tungependa kushauri ni namna bora na haraka kwa sababu sasa hivi tuko kwenye msimu basi waraka utoke mapema ili Vyama vyetu vya Msingi na Ushirika viweze sasa kupkea maagizo haya na tuanze kutekeleza wakati tunakusudia kwenda kuimarisha na kuwainua wananchi wetu kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ni eneo la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji, hili ni jambo zuri na tayari tumeona kwenye bajeti kiasi cha pesa ambacho kimetengwa. Ushauri ambao ningependa kuutoa kwa Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha ni kwamba kwa Jimbo kama Nachingwea nina jumla ya vijiji 127 nikipiga hesabu kwa shilingi milioni 50 kwa vijiji hivi maana yake Nachingwea pekeyake tunaweza kupata zaidi ya shilingi bilioni sita karibu na milioni 300. Nachingwea imejaliwa kuwa na ardhi kubwa sana sijajua ni mfumo gani tunakwenda kuutumia ingawaje tayari tumeshaanza kuona suala la kuundwa kwa SACCOS mbalimbali bado nina mashaka namna ambavyo fedha hizi zitakavyokwenda kuwanufaisha Watanzania walio wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa yale maeneo ambayo yamejaaliwa kuwa na rasilimali kama ardhi na wananchi wake wanautashi wa kushiriki kwenye kilimo nilifikiri Serikali ingefikiria mara mbili namna ya kuweza kuzigawanya fedha hizi ili ziweze kuleta tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, na ushauri huu narudia kwa mara ya pili kuutoa hata kama hauwezi kufanyiwa kazi. Nilikuwa nashauri kwa yale maeneo ambayo yana interest ya kilimo ni bora hizi pesa zikaletwa tukanunua matrekta. Kwa Wilaya yangu kwa idadi ya vijiji nilivyokutajia tukipata matrekta 127 sasa hivi Wilaya nzima matrekta hata kumi hayazidi, wananchi wakati huu wakuandaa mashamba wanapata shida.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo pesa hii badala ya kupelekea vikundi tungepeleka katika vyama vyetu vya Ushirika au utaratibu mwingine wowote ili waweze kununua matrekta ambayo yatarahisisha wananchi kutibulisha maeneo yao kwa gharama nafuu na hivyo tunaweza kuongeza kipato kwa wazalishaji wa kilimo na pia tunaweza sasa kuongeza jitihada na kutimiza ndoto zetu katika lile lengo la kuwa na viwanda ambavyo kwa sehemu kubwa vinategemea malighafi kutoka kwenye eneo la kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ambalo ningependa kulizungumzia ni eneo la nishati, nimesoma kitabu cha mpango wa uchumi, nimeangalia kanda mbalimbali namna ambavyo zimejipanga katika kuboresha uchumi wa maeneo husika. Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Mtwara sasa hivi ndio unaongoza kwa kutoa gesi ile ya Songosongo lakini gesi ya Mnazi Bay, lakini kwa sehemu kubwa bado nimeangalia kanda za madini ambazo zimetajwa katika Taifa letu, katika kanda hizi kwa bahati mbaya sijaona kanda hata moja kutoka Mikoa ya Kusini wakati sasa hivi kuna gypsum inapatikana maeneo ya Lindi, kuna madini yanapatikana maeneo ya Nachingwea, kuna madini yanapatikana ukanda mzima wa gesi kwa maana ya pale Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, bado katika kanda hizi za Kitaifa bado Mikoa ya Lindi na Mtwara hajatambulika, ingawa kuna hii LNG plant ambayo nimeona nayo pia Serikali imeweka mkakati wa kwenda kuboresha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wakati unakuja kutoa hitimisho tunaomba ufafanuzi wa kuona namna gani katika kuboresha uchumi wa Taifa letu watu wa Mikoa ya Lindi na Mtwara ni kwa kiasi gani wanakwenda kunufaika na rasilimali hii ambayo imekuwa inatoa huduma Tanzania nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo uchumi wetu hauwezi kwenda vizuri katika Mikoa ya Lindi na Mtwara kama hatuwezi kuboresha huduma ya nishati ya umeme. Bado tuna tatizo la umeme katika Mikoa yetu pamoja na kwamba gesi inatoka katika Mikoa hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Wizara ya Nishati tunampongeza Mheshimiwa Profesa Muhongo kwa jitihada anazozifanya, lakini tunaomba kupitia bajeti yetu hii basi vijiji vyetu viende kupata umeme wa uhakika lakini pia viende kuboresha viwanda ambavyo tumeshaanza kuwa navyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunacho kiwanda cha Dangote pale Mtwara lakini bado wakazi wa Mikoa ya Lindi naMtwara hawajanufaika kwa sehemu kubwa na kiwanda hiki kutokana na bei kuwa kubwa ya cement ambayo inazalishwa pale. Sasa bado wananchi wetu wako chini kiuchumi na hatuwezi kuwasaidia kama tunawauzia kwa bei kubwa wakati Dar es salaam na maeneo mengine wanapata kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumza hayo naomba niunge mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kutoa shukrani kwako kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu naomba nijielekeze katika maeneo makubwa matatu. Eneo la kwanza ambalo ningependa kuligusia kwa umuhimu wake ambalo hili linaunganisha maeneo yote ni eneo la elimu. Nimepitia vizuri mpango, naomba nitoe pongezi kwa yale ambayo tayari yameshafanyika ndani ya kipindi hiki lakini bado kuna maeneo ambayo nilifikiri kuna umuhimu wa kuelekeza nguvu na kuona namna gani tunaweza kuweka maboresho zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni uboreshaji wa miundombinu. Tayari tumeona utekelezaji wa upatikanaji wa elimu bure katika shule zetu za msingi pamoja na sekondari, lakini bado kuna tatizo kubwa za vyumba vya madarasa katika shule zetu lakini pia kumekuwa na matatizo makubwa katika upatikanaji wa nyumba za Walimu. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika mpango huu ambao tunaujadili sasa eneo hili ni lazima lioneshwe wazi ni kwa kiasi gani tunakwenda kuboresha miundombinu hii ili kuunga mkono kile ambacho tayari kimeshafanyika katika eneo hili la kutoa elimu bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sera yetu ya kuboresha viwanda wataalam watapatikana kupitia elimu, lakini bado kuna umuhimu wa kuangalia namna gani tutahusianisha maendeleo yetu pamoja na elimu ambayo tunaitoa kwa vijana wetu katika shule zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie upande wa elimu ni suala zima la mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa ambapo sisi kama Wabunge lazima tuishauri vizuri Serikali yetu ili iweze kuendelea kutoa mikopo kwa vigezo vile ambavyo vilishakuwa vinatumika. Yako marekebisho, upo upungufu tulishazungumza hapa mwaka jana lakini kuna umuhimu sasa wa hiki ambacho kinafanyika sasa hivi kuangaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Serikali kwa ujumla lazima ifanye jitihada za makusudi kuingilia kati ili kuhakikisha watoto wa wakulima ambao leo hii wanafukuzwa vyuoni bila sababu za msingi wanapata mikopo ili waweze kupata elimu, ambapo hawa ndiyo tutakwenda kuwatumia baadaye katika viwanda ambavyo tunasema tunataka kwenda kuviboresha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili naomba pia nimshauri Mheshimiwa Waziri, hebu wachukue jitihada za makusudi kuiangalia Bodi ya Mikopo. Sasa hivi wamekuja na vigezo ambavyo vitakwenda kuwabana watoto wetu kwa kiasi kikubwa sana. Wametengeneza fomu ambazo kimsingi ukiangalia kwa undani vigezo ambavyo wanakwenda kuviweka bado haviendi kumsaidia mtoto wa mkulima ambaye kwa kweli sehemu pekee ya kukimbilia ni katika Serikali ili waweze kupata mikopo ambayo itaenda kusaidia kuzalisha wasomi katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka nichangie ni la kilimo. Naomba niungane au nitoe salamu kutoka kwa wananchi wa Jimbo la Nachingwea na Kusini kwa ujumla. Kwa muda mrefu tulikuwa tunajadili kero ambazo tumekuwanazo kwenye zao la korosho sasa hivi korosho imekuwa na uchumi mkubwa sana. Serikali imeondoa tozo tano ambazo sisi tulizijadili hapa katika mpango huu mwaka jana. Katika hili Mheshimiwa Waziri naomba tuwapongeze sana kwa kusikiliza kilio chetu, tumeweza kuondoa kodi. Leo hii tunavyozungumza mkulima anapima korosho yake kilo moja shilingi elfu tatu mpaka elfu tatu na mia nane, hili ni jambo zito, ni jambo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu naomba tuharakishe katika suala zima la malipo kwa wakulima wetu mara baada ya kuwa minada imeshafanyika. Leo hii nazungumza kwenye Wilaya yangu ni zaidi ya siku nane mnada umeshafanyika bado wakulima wanaendelea kupata shida malipo yao hawajapata. Hii itaenda kusababisha chomachoma kuendelea kuwadhulumu wakulima kitu ambacho Serikali tayari ilishapiga hatua katika eneo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie katika eneo hili la korosho au katika eneo la kilimo ni suala zima linalohusiana na utendaji wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Serikali inapoteza mapato mengi sana katika eneo hili. Ukiondoa korosho ambayo leo kwetu imekuwa ni uchumi mkubwa bado tuna mazao kama ya ufuta, mbaazi ambayo mwaka jana na mwaka huu tumeuza kwa bei ya chini sana na hii ni kwa sababu Bodi ya Mazao Mchanganyiko haifanyi kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapoteza kodi hapa, Halmashauri zetu zinapoteza kodi, lakini wakulima wetu pia wanapoteza fedha nyingi ambayo tulifikiri ingeweza kuwasaidia. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri anapokwenda kujumuisha, anapokwenda kushauriana na wenziwe tunaomba katika eneo hili tusaidiane na watu wa Wizara ya Kilimo ili tuhakikishe Bodi ya Mazao Mchanganyiko inafanya kazi ili tuweze kukusanya kodi zaidi ambayo itasaidia katika eneo hili la kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala zima la upatikanaji wa pembejeo. Pembejeo bado hazipatikani kwa wakati. Hapa tunavyozungumza sasa hivi msimu wa kilimo umeanza lakini mpaka sasa hivi bado pembejeo kwa wakulima wetu hazina uelekeo mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri, hatuwezi kujadili kuwa na viwanda kama hatuwezi kujadili namna ya kuwa na kilimo bora. Kilimo bora tutakipata kwa kuwapelekea wakulima pembejeo kwa wakati na vitendea kazi vingine ambavyo vitawasaidia. Kwa hiyo, nafikiri ni muhimu tuishauri Serikali ili iweze kuboresha katika eneo hili ambalo kimsingi litakwenda kuwasaidia wakulima wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine katika kilimo ni suala zima la kufufua na kuchukua viwanda ambavyo tayari vilishachukuliwa na wawekezaji. Ndani ya Wilaya yangu ya Nachingwea tuna viwanda viwili, kimoja cha korosho lakini tunacho kiwanda kimoja cha kukamua mafuta. Naomba nimshukuru kwa upekee Mheshimiwa Waziri Mkuu amefanya ziara katika haya maeneo, Serikali haina sababu ya kupoteza muda ichukue hivi viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yale majengo sasa hivi yanatumika kwa matumizi ambayo hayakukusudiwa, vipuri vinaendelea kung’olewa katika vile viwanda. Leo hii tunahitaji kuwa na processing industries kwa hizi korosho tunazozalisha. Tungefurahi kuona Serikali yetu kwa hii sera ya kuwa na viwanda inaenda kuchukua hivi viwanda ili tuweze sisi wenyewe kuandaa korosho zetu, ufuta wetu kwa bei nafuu ambayo tunafikiri itakwenda kuleta tija kwa mkulima badala ya sasa hivi kuuza korosho na ufuta kwenda nje ya mipaka yetu kufanyiwa processing.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala zima linalohusu nishati. Hatuwezi kuwa na viwanda, hatuwezi kufanya lolote kama nishati ya umeme bado ni tatizo. Mikoa yetu mingi bado umeme wa uhakika hatuna. Kwa hiyo, naomba Waziri atakapokwenda kuhitimisha na kupitia mpango wake lazima aseme tatizo la umeme katika Majimbo yetu na Wilaya zetu linakwenda kupatiwa ufumbuzi kwa namna gani? Hili ni lazima lionekane katika mpango badala ya kuwa katika ujumla wake kama ambavyo imeonesha hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nafasi hii, naomba nikushukuru sana na naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru sana kunipa nafasi niweze
kuchangia. Naomba nitoe pongezi, lakini pia niwapongeze Mawaziri wote kwa kazi nzuri
ambayo wanaendelea katika uwasilishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwangu mimi ni maeneo mawili makubwa. Jambo la
kwanza ni suala la umeme. Wajumbe wenzangu waliotangulia wameshazungumza sana lakini
kwa kuonesha msisitizo na kwa kuonesha tatizo ambalo mikoa yetu ya Lindi na Mtwara
tunakabiliwa nalo naomba nilirudie pia kulizungumza.
Mheshimiwa Naibu Spika, umeme Mkoa wa Lindi na Mtwara ni tatizo, kwa siku umeme
unakatika si chini ya mara saba mpaka mara nane. Kila Mbunge anaesimama anaetoka Lindi
na Mtwara jambo hili amekuwa analiulizia na kulitolea ufafanuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba pamoja na jitihada na kazi zote
zinazoendelea kufanyika, suala la umeme, kile kituo ambacho tumeahidiwa kitajengwa pale
Mnazi Mmoja kwa ajili ya kusambaza umeme katika maeneo ya Kanda nzima tunafikiri sasa ni
wakati muafaka wa kuweza kulitekeleza jambo hili. Kwa kufanya hivyo tutaendana sambamba
na kauli ya kujenga uchumi kupitia viwanda ambavyo tunaendelea kuvihamasisha. Nje ya
hapo kwa kweli hali itaendelea kuwa mbaya na watu wetu kwa kweli wanaendelea kupata
shida wakati hatuna sababu ya kupata shida ukizingatia gesi sasa hivi kwa sehemu kubwa
inatoka katika ukanda wa kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili katika umeme ni suala la umeme vijijini. Naomba
niishukuru Serikali, kwa awamu ya pili vijiji vingi vya Wilaya ya Nachingwea vimepata umeme,
lakini nilikuwa naomba katika hii Awamu ya Tatu basi ni vizuri, kama ambavyo wenzangu
wametangulia kusema msisitizo uweze kuanza ili vijiji vilivyobakia katika Tarafa tano za Wilaya ya
Nachingwea viweze kupatiwa umeme wa uhakika ili wananchi waweze kupata huduma
ambayo kimsingi inahitajika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu ni suala la barabara. Mwaka jana tumezungumza
habari ya barabara, lakini mwaka huu tunapokwenda kuanza kutekeleza mambo yetu
ingawaje tuko ndani ya bajeti bado kuna umuhimu wa kujenga barabara kwa kiwango cha
lami. Hapa naomba niizungumzie barabara ya Masasi - Nachingwea, Nachingwea -
Nanganga, ni kilometa 91. Jambo hili wananchi wa Jimbo la Nachingwea, Masasi pamoja na
maeneo ya jirani limekuwa linatunyima raha sana na limekuwa linatuchelewesha kwenye
shughuli za maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri pamoja na watu wa
Wizara katika utaratibu tunaoenda kuuweka basi kwa sababu tayari feasibility study imefanyika,
tunaomba barabara hii watu wa Mkoa wa Lindi, watu wa Wilaya ya Nachingwea tuweze
kupatiwa ili tuweze kujikwamua kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia ni suala
la madini. Mheshimiwa Naibu Waziri, mwaka wa jana niliuliza swali hapa alinipa takwimu ya
makampuni zaidi ya 240 yanayofanya utafiti katika Mkoa wa Lindi, lakini baada ya kufuatilia
mpaka sasa hivi makampuni haya yote ambayo yametajwa katika orodha yao sijaona kampuni
hata moja inayoendelea na utafiti wa madini katika maeneo yetu. (Makofi)
Kwa hiyo, nilikuwa naomba kutoa masisitizo, wananchi wanataka wapate fursa ya
kuchimba madini katika maeneo yanayozunguka Nachingwea, lakini bado jitihada za utafiti
hazijafanyika. Kwa hiyo, nitoe msisitizo, yale makampuni yaliyotajwa tunaomba yaje na tuyaone
bayana ili tuweze kuwasaidia kuwaonesha maeneo gani tunaweza tukapata madini na hivyo
tuweze kusaidia vijana wetu kupata ajira wajikwamue kupitia shughuli zao za kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na muda naomba niseme hayo lakini pia naomba
niunge mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Waziri wa Elimu. Naomba nizungumzie mambo makubwa matatu. Jambo la kwanza ni kuipongeza Serikali, kuwapongeza watendaji pamoja na watumishi wote wa Wizara hii wakiongozwa na mama yetu, Mheshimiwa Ndalichako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo mengi sana ambayo yamefanyika, kwangu binafsi kwa niaba ya wananchi ambao ninawawakilisha hapa, nitakuwa mtovu wa fadhala kama sitatambua kazi kubwa ambayo wameifanya ndani ya Jimbo la Nachingwea hasa katika eneo hili la elimu. Uko uboreshaji mkubwa wa Chuo cha Walimu Nachingwea umetumia gharama kubwa sana na sasa hivi mazingira yamekuwa ni yakuvutia sana watu kuendelea kupata elimu katika eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niunganishe na ombi moja kwa moja hapo hapo, pamoja na jitihada zile bado tunaomba pia tupate fedha kwa ajili ya kukarabati nyumba za watumishi katika eneo lile au katika taasisi ile Chuo cha Uwalimu Nachingwea. Nyumba zilizopo bado siyo nzuri na hazivutii, lakini gharama yoyote ambayo mtakuwa mmetusaidia, basi mtakuwa mmeyaweka mazingira yale yawe ya kuvutia zaidi na hivyo kutoa elimu ambayo tunaikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo pia nilitaka nipongeze ni suala zima la ajira mpya kwa walimu. Tunaishukuru sana Wizara, tumepata mgao wa walimu ingawa bado hawatoshi na changamoto kubwa tunayo katika eneo la walimu wa sayansi. Walimu ambao tumepatiwa kwa mahitaji ilikuwa ni 30 lakini tuliopokea ni chini ya asilimia 50. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri na wataalam wakeo hebu walione hili ili waweze kutusaidia tupate walimu wa kutosha ambao wataenda kutoa maarifa kwa vijana wetu katika shule zetu za Wilaya ya Nachingwea na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nilitaka nichangie kupitia hotuba hii linalohusu namna ya kuwaendeleza walimu. Ukiangalia kada mbalimbali za Utumishi, ipo mifumo ambayo inawa-favour watumishi tofauti na kada ya walimu. Katika level za Form Four ambazo wamekuwa wanatumia vyeti kupata elimu ya ngazi ya cheti, wenzetu wa kada nyingine wamekuwa wanatumia vyeti hivyo kwa ajili ya kupata Diploma na Degree, lakini kwa upande wa walimu, nafikiri kwa wale walimu watakubaliana name; tumekuwa na changamoto kutoruhusu walimu wetu kutumia vyeti vya Form Four au vyeti vya certificate kutoka Grade A mathalani kwenda kupata ngazi nyingine ikiwemo Diploma au Degree.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu wataalam wa Wizara ya Elimu wakae walione namna bora ambavyo tunaweza nayo pia tuka-switch na tukatengeneza utaratibu ambao utasaidia walimu au wale wanaojiendeleza na ualimu kutumia certificate kwenda ngazi nyingine za juu ili kuondoa urasimu ambao kwa sasa hivi upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua imefanyika hivi kutokana na umuhimu wa kada ya elimu na labda lengo lake ni ku-impart knowledge zaidi kwa walimu ili waweze kuwa walimu wazuri, lakini bado naamini mafunzo na mitaala ambayo wanaitumia kupata elimu yao, bado inaweza ikasaidia walimu hawa kujiendeleza na kupata elimu ya juu zaidi ya vyeti ambavyo wamekuwa navyo katika wakati tulionao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nilitaka nichangie katika hotuba hii ni suala zima linalohusu gharama za uendeshaji katika vyuo vyetu. Serikali imefanya kazi kubwa ya kuboresha mazingira ya vyuo na sasa hivi vyuo vingi vikongwe vinapata huduma muhimu. Hata hivyo, bado zipo changamoto za kuhakikisha vyuo hivi vinajienda vyenyewe. Vyuo vingi sasa hivi wana changamoto ya kupata fedha kwa ajili ya kulipia umeme; vyuo vingi sasa hivi vinapata changamoto kubwa sana kwa ajili ya kupata fedha kwa ajili kugharamia na hata kulipia bili za maji. Yote haya ni kwa sababu Serikali kupitia kukusanya maduhuli, ikiwemo ada na vitu vingine, gharama hizi zote zimekuwa zinaenda Serikali. Kwa hiyo, mgao ambao wanarudisha katika vyuo vyetu haukidhi mahitaji ya vyuo vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwa heshima na taadhima Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalamu wake hebu walione hili, badala ya kuendelea kuwakatisha tamaa Wakufunzi ambao wako katika vyuo hivi vya kati au Vyuo hivi vya Ualimu, tuone namna tunavyoweza kurudisha sehemu ya gharama ili waweze kumudu gharama mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia hili kwa experience ya chuo ambacho nimekitaja, mara nyingi nimekuwa nawasiliana nao, nimeona namna wanavyohangaika kulipia sehemu ya gharama ambazo kimsingi zamani ilikuwa moja kwa moja wao vyuo ilikuwa na mamlaka ya kukusanya na kuweza kutumia moja kwa moja. Kwa hiyo, niliona hili nalo niliwasilishe kama sehemu ya changamoto na pia nipendekeze kwa Serikali ione namna bora ya kuweza kuliangalia hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo nilitaka nichangie katika Wizara hii ni suala nzima linalohusu gharama kwa ajili ya wanavyuo walioko katika hivi Vyuo vya Ualimu. Kwa mwaka sasa hivi wanafunzi wanalipa siyo chini ya shilingi 600,000/=. Nia njema ya Serikali kutoa elimu bure ambayo tunaiunga mkono na imeleta mafanikio makubwa sana, imeanza katika ngazi ya shule za msingi, tumekwenda mpaka sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipato cha Watanzania hawa ambao tumekuwa tunawapa elimu bure kuanzia msingi kwenda sekondari, bado kumekuwa na changamoto ya namna wanafunzi wanavyoweza kugharamia sehemu ya malipo kwa ajili ya kulipia hii Elimu ya Ualimu. Kwa hiyo, nimefanya utafiti kwenye baadhi ya vyuo, wanafunzi wengi wanashindwa kugharamia hizi gharama na imekuwa inaleta usumbufu kidogo katika kukamilisha mafunzo au masomo ambayo wamekuwa wanayapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na Serikali kuwa na mzigo mzito wa kukopesha wana vyuo katika ngazi mbalimbali za Degree na Shahada mbalimbali naomba nitoe ushauri kwa watu wa Wizara waone kama kuna uwezekano pia wa kuwaangalia hawa Watanzania ambao kwa sehemu kubwa wamenufaika na elimu bure mpaka wanavyofika katika ngazi hii ya elimu ya kati ambayo tukiweka masharti nafuu ya kuweza kuwafanya hawa wamalize vyuo vyao, basi tutakuwa tumejikuta tume-groom walimu wa kutosha ambao watakwenda kutoa elimu moja kwa moja katika maeneo yetu na hivyo tatizo la walimu litaenda kupungua kwa kiasi kikubwa sana. Jitihada hizi za Serikali ambazo zinafanyika, sisi tunaendelea kuziunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho kabisa, nizungumzie suala linalohusiana na mgawanyo wa hawa walimu ambao tulikuwa tunawatawanya. Ukienda kwenye maeneo ya Sekta za Utalii, watu kama wa Kilimanjaro huwa wananufaika kwa sehemu kubwa sana na mgao ambao umekuwa unapatikana na vyanzo vile vya utalii na vitu mbalimbali. Hata hivyo, katika maeneo ambao kumekuwa na vyuo ndiyo maeneo ambayo yamekuwa yanaongoza kwa kutokuwa na walimu wa kutosha. Wilaya kama Nachingwea mathalani, ni jambo la ajabu sana kukosa walimu hasa katika level za shule za msingi. Hapa tuna upungufu mkubwa sana, lakini walimu wengi wanazalishwa pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, najua hivi vyuo ni vya Kitaifa na tunazalisha hawa walimu kwa ajili ya kuhudumia Taifa zima. Naomba tufanye upendeleo wa makusudi katika maeneo ambapo vyuo vipo, basi angalau tuone tunanufaika kwa kiasi kikubwa. Kwa hili, naomba nilete ombi kwa Mheshimiwa Waziri aiangalie Wilaya ya Nachingwea, mgao ambao tumepatiwa safari hii bado hauakisi idadi ya shule tulizonazo na wingi wa shule ambazo tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii imetupa changamoto ya namna kutoa elimu ambayo kimsingi tumekuwa tunaikusudia. Kwa hiyo, ebu tutumie chuo kile kilichopo Nachingwea kutupendelea kidogo ili tuweze kupata walimu ambao watatoka moja kwa moja pale na hasa wale ambao wametoka katika shule jirani kutoka maeneo yale ya Chuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatufanyi hivi kwa maana ya kuwabagua watu wengine, lakini ni ukweli ambao utakubaliana name, lazima moto unapodondokea kwenye mkono, basi yule ambaye umemdondokea aanze kujitoa yeye mwenyewe kabla ya mtu mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliomba nichangie hayo kwa ufupi sana ili kuweza kuboresha bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimia Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kuniona. Bila kupoteza muda naomba pia niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pole kwa ndugu zetu ambao wamepoteza wapendwa wetu kule Mkoani Arusha. Pia naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri ambayo anaifanya ya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naungana na kaka yangu kiongozi wangu Mzee Bulembo kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kumchagua Profesa Kitila, Mwalimu wangu. Naomba nimtakie kazi njema ya kututumikia Watanzania, naamini hutotuangusha katika kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika mambo machache yanayohusu eneo la Jimbo langu la Nachingwea. Mheshimiwa Waziri pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa nyakati tofauti wamefika katika Jimbo la Nachingwea, wameona hali ya upatikanaji wa maji katika vijiji vya Jimbo la Nachingwea. Hapa kuna mradi mkubwa wa Mbwinji ambao unahudumia Wilaya ya Masasi, Wilaya ya Nachingwea pamoja na Wilaya ya Rwangwa.

Mheshimia Naibu Spika, iko ahadi, vile vile iko fedha ambayo mwaka 2016 tulitengewa kwa ajili ya kusambaza maji katika vijiji ambavyo viko umbali wa kilomita tano. Naomba kupitia nafasi hii, niwakumbushe juu ya hali ya upatikanaji wa maji katika vijiji vinavyozunguka Jimbo la Nachingwea. Tafadhali sana naomba wayafanyie kazi maombi ambayo tayari yako katika ofisi yao kwa ajili ya kutoa fedha ambayo tayari ilishapitishwa katika bajeti iliyopita ili tuweze kuwapa wananchi maji ya uhakika na maji salama ambapo wamekuwa wanapata shida kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya Naipanga, Mkotokwiana, maeneo ya Chemchem, ni maeneo ambayo wanaathirika kwa kiasi kikubwa sana. Kwa hiyo, utekelezaji wowote utakaofanyika, basi tutakuwa kweli tumekwenda kuwatua mama zetu ndoo kichwani kwa ajili ya kuwapunguzia adha wanayoipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nizungumzie ni suala la ulipaji wa bili za umeme. Ndani ya Wilaya yangu ya Nachingwea, zaidi ya wiki mbili tumekaa bila kupata maji kwa sababu ya umeme, ambapo kimsingi siyo kosa la wananchi. Wananchi wanalipa bili zao, lakini wamelazimika kukaa bila maji kwa sababu tu Wizara imeshindwa kulipia bili ambazo kimsingi wananchi hawahusiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri pamoja na timu nzima kwamba jambo hili kwa kweli tusingependa lijurudie kwa sababu tunawapa adhabu wananchi ambao wao wanatimiza wajibu wao wakulipia bili zao za maji. Kwa Wilaya ya Nachingwea peke yake kupitia MANAWASA, zaidi ya shilingi milioni 100 zinatakiwa zilipwe. Kwa hiyo, naomba tafadhali hiyo fedha ilipwe ili wananchi wa Jimbo la Nachingwea waweze kupata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ambalo nataka nimkumbushe Mheshimiwa Waziri wa Maji, kupitia Naibu Waziri ambaye alishakuja Jimboni Nachingwea, alikuja katika Kijiji cha Chiola, nafikiri anakumbuka ule mradi; na kuna ahadi ambayo aliitoa na wale wananchi wananiulizia: Ni lini utekelezaji wa yale ambayo tayari aliyaahidi pale ya kuleta wataalam kuja kuchunguza ule mradi? Ni lini tutakwenda kuukamilisha? Sina majibu, namwomba mzee wangu kwa sababu tumefanya kazi nzuri katika Jimbo hili, tafadhali sana anisaidie ili wale wananchi waweze kupata maji ya uhakika na maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ambalo nataka nilizungumzie ni suala la Miradi ya Umwagiliaji. Katika Jimbo la Nachingwea, tunayo miradi miwili; tunao Mradi wa Matekwe, huu ulishapewa fedha kipindi cha nyuma zaidi ya shilingi milioni 500, lakini mpaka sasa hivi mradi huu sijauona hata kwenye kitabu unatajwa kwa namna yoyote; sijui kama umefutwa! Zile fedha zilizotolewa kama zimepotea, basi tunaomba tuelezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti hii. Naomba niungane na wenzangu waliopita, kumpongeza Mheshimiwa Waziri, lakini pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuwafanyia Watanzania, ya kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nijielekeze katika maeneo makubwa manne. Eneo la kwanza ambalo nilitaka nichangie ni eneo la kilimo. Kwa niaba ya wananchi ambao nawawakilisha naomba nifikishe salamu zao za pongezi kwa kilio cha muda mrefu cha kuwaondolea adha kubwa ya tozo katika zao kubwa ambalo linatuletea uchumi mkubwa katika maeneo yetu, zao la korosho. Kwa muda mrefu tumekuwa tunalalamikia tozo nyingi ambazo zilikuwa zinapunguza bei ya korosho, lakini kwa sasa kupitia Rais wetu wakulima wa zao la korosho wamenufaika kwa kiasi kikubwa. Ndani ya Wilaya ya Nachingwea, Liwale na Ruangwa kwa mwaka huu peke yake si chini ya shilingi bilioni 46 zimeingia katika mzunguko wa fedha za wakulima. Hii ni kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo, naomba nizungumzie nakupongeza pia suala zima la kutoa pembejeo bure, sulfur pamoja na madawa mengine ili kuweza kukuza zao hili la korosho. Changamoto kubwa ambayo nilitaka nishauri kupitia kwa Waziri wa Kilimo na Wizara kwa ujumla ni suala zima la kuangalia pembejeo hizi zinapatikana kwa wakati gani. Mpaka sasa hivi ninapozungumza tayari wakulima wanahitaji kuona pembejeo zimeshawafikia, lakini bado kuna baadhi ya maeneo pembejeo kwa maana ya sulfur mikorosho imeshaanza kutoa maua bado sulfur haijafika. Kwa hiyo, niombe haraka iwezekenavyo Wizara ipeleke sulfur katika maeneo ya mikoa ya Lindi, Mtwara, ili wakulima waweze kupulizia mikorosho yao tuweze kuuwahi msimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, pamoja na nia nzuri ya Serikali ya kutoa sulfur bure bado kuna changamoto ya uchache wa sulfur hii ambayo inaenda kutolewa kwa wakulima. Mpaka sasa hivi nazungumza kwa Wilaya ya Nachingwea peke yake ina mgao wa tani 1300, kwa idadi ya wakulima na uzalishaji wa Wilaya ya Nachingwea peke yake idadi hii ya pembejeo ambayo tunaenda kupata ni ndogo na haiwezi kukidhi mahitaji. Kwa hiyo naomba Wizara naomba Serikali iongeze idadi ya mgao ili wakulima wengi waweze kupata sulfur na pembejeo za kutosha ili waweze kuhudumia mikorosho yao tuweze kuingia katika Kilimo kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nilitaka nizungumze ni suala zima la maboresho ambayo tungependa yafanyike pia ili kumnufaisha mkulima. Tunahitaji tuone utekelezaji wa kuanza kazi kwa bodi ya mazao mchanganyiko. Ukiondoa korosho ambayo inatuletea uchumi mkubwa, bado tuna mazao ya mbaazi, tuna mazao ya choroko, lakini pia tuna mazao ya ufuta ambayo muda si mrefu tunaenda kuingia kwenye msimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu tumepigia kelele kuona bodi hii inafanya kazi lakini mpaka sasa hivi bado Serikali imekuwa na kigugumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Wizara, naomba nishauri Serikali ione umuhimu wa Bodi ya Mazo mchanganyiko iweze kufanya kazi kuanzia mwaka huu ili iweze kusimamia bei ya wakulima wetu katika haya mazao mengine ambayo wakulima wetu wameitikia wito wa kulima kwa nguvu na kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo ningependa nizungumzie, unapozungumza uchumi na unapozungumza kuiunganisha Tanzania, unapozungumza suala la viwanda, huwezi kusahau suala zima la umeme. Bado mikoa yetu ya Lindi na Mtwara ina matatizo makubwa ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka leo tunazungumza, Serikali imeonyesha nia ya kujenga kituo pale Mnazi Mmoja. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie wametenga kiasi gani na wana nia gani ya kwenda kuhakikisha mitambo ile inaanza kufanya kazi ili wananchi wa kule waweze kupata umeme wa uhakika, ambao wataweza kuzalisha kwa ufanisi na kutosimamisha shughuli za maendeleo ambazo mpaka sasa imekuwa ni kitendawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nilitaka nizungumzie ni suala zima la barabara. Nimepiga kelele toka mwaka jana, nimepiga kelele mwaka huu. Kwenye bajeti ya mwaka huu ya Wizara tumeahidiwa kutengewa bilioni tatu; lakini bado ningependa kuona Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha, kwa uchumi ambao mikoa hii inazalisha, tungependa kuona barabara ya Masasi - Nachingwea na Nganga, lakini pia sasa hivi tunazungumzia barabara ya Ruangwa, fedha hii ambayo imeahidiwa inaenda kupatikana kwenye fungu gani na lini fedha hii inaenda kutoka ili tuanze ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, ambayo nayo imekuwa ni kikwazo kikubwa cha maendeleo katika ukanda huu kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo naomba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maelezo ambayo Mheshimiwa Waziri ameyatoa katika hotuba yake, na katika vipaumbele ambavyo vimepangwa hivi vinne, nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza yeye pamoja na ofisi yake, lakini pia niipongeze Serikali kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wanaifanya kwa ajili ya kuhakikisha Watanzania wanapata maendeleo. Sambamba na haya, yapo maeneo ambayo ninapenda nitumie nafasi hii kumshauri Mheshimiwa Waziri na wadau wote ambao wanahusika katika kuendelea kutuletea shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapojadili viwanda huwezi kutenganisha na suala zima la kilimo. Moja ya vipaumbele vikubwa ambavyo tumeviweka kwenye mpango ni suala la uendelezaji wa viwanda vyetu. Kazi kubwa Mheshimiwa Rais wetu amekuwa anaifanya ya kuhakikisha tunafufua viwanda ambavyo vime-cease kufanya kazi, lakini pia kuhakikisha tunaleta wawekezaji wengine ambao wanafungua viwanda vipya, lakini bado zipo changamoto ambazo nilikuwa naziona; watu wa Wizara ambao wanatuwekea mipango hii lazima pia waangalie vipaumbele vyao waelekeze katika maeneo ambayo tayari tumeshaanza kuchukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika upande wa kilimo wa zao la korosho Ukanda wa Kusini, Mikoa ya Lindi na Mtwara kwa sasa hivi shughuli kubwa ambayo inatuingizia kipato ni zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji wengi wako kule, makampuni mengi yako kule, lakini pia hata kipato cha wananchi wetu kwa kipindi kama hiki kinakuwa ni kikubwa sana, lakini uwekezaji gani tumeufanya sisi kama Serikali ninafikiri ni jambo ambalo Wizara lazima sasa waaangalie na waelekeze nguvu zao na macho yao ili kuhakikisha zao hili linafanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie nafasi hii kuishuru Serikali, mwaka jana kuja msimu huu wametusaidia kutua sulfur kwa ajili ya kuhakikisha tunafanya uzalishaji mkubwa. Hata hivyo bado ninaomba niishauri Wizara au nimshauri Mheshimiwa Dkt. Mpango waone umuhimu sasa wa kufungua kiwanda ambacho kitakwenda kuzalisha sulfur katika Mkoa wa Lindi. Sulfur hii itasaidia wakulima wengi wa maeneo yote ya mkoa na wale wote wanaotumia kulima zao hili waweze kupata huduma ya pembejeo kwa karibu na kwa gharama nafuu zaidi. Msimu huu tumepata bure, lakini bado tumekuwa na changamoto ya uchache wa sulfur tuliyopokea, lakini pia tumepata changamoto ya kuchelewa kwa sulfur ambayo kimsingi imeshusha kidogo uzalishaji wa zao hili kubwa la biashara ambalo sasa hivi angalau tunaweza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe katika eneo hili la uwekezaji katika viwanda, moja ya vipaumbele vyetu hebu tuangalie namna ambavyo tunaweza tukatengeneza kiwanda cha sulfur na mipango hiyo tayari ilishakuwepo, muhimu ni kuanza utekelezaji. Kwa hiyo katika bajeti zetu na mipango yetu ninaomba hili wazo nililete ili tuweze kulipa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili katika kilimo ni suala zima la uanzishwaji pia wa viwanda vya magunia au vifungashio. Sasa hivi tunapata magunia kutoka nje, tunapata magunia kutoka maeneo ya mbali, hii imeleta shida sana pia kwa wakulima wetu katika msimu kama huu. Hii ni fursa nyingine ambayo Serikali ingeweza kutengeneza fedha kubwa sana kupitia utengenezaji wa kiwanda ambacho kitaenda kutoa magunia na kwa sababu mahitaji ni makubwa, basi ninaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha aone umuhimu sasa wa kuelekeza nguvu katika eneo hili la viwanda tuweze kupata kiwanda ambacho kitazalisha magunia na vifungashio vyote ambavyo vitawasaidia wakulima wetu wa zao hili la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu katika kilimo, ninapenda pia kuzungumzia suala la kilimo cha mbaazi. Hili zao kwa muda mrefu tumekuja hapa Bungeni, tumelalamikia na kutoa maelekezo lakini bado majibu ya kutosheleza mpaka sasa hivi hatujapata. Leo hii ukienda katika Jimbo la Nachingwea kwa msimu mzima wakulima wamejitokeza, wamelima mbaazi nyingi sana ambao sasa hivi hazina soko na hazima kazi yoyote ya kufanya, lakini bado nasikitika kusema Wizara mpaka sasa hivi hawana kauli yoyote ambayo wameitoa juu ya zao hili la mbaazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha, lakini pia Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, kaka yangu, Mheshimiwa Dkt. Tizeba ni muhimu sasa atoke na atoe tamko rasmi la kusema nini hatma ya zao la mbaazi kwa wakulima wetu ambao tuliwahamasisha, wakajitokeza kuchukua muda wao, lakini pia wakaongeza mashamba yao na kulima zao ambalo mikataba imevunjwa, soko hakuna. Sasa hivi mbaaza kilo shilingi 150, shilingi 200, lakini nilitegemea Serikali itasema kwamba kama tumekosa wanunuzi ambao tulikuwa tunawategemea kutoka India nini mbadala wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama mwakilishi wa wananchi na kwa sababu wananchi wenyewe wanatusikiliza sasa tunafika wakati tunapata uvivu hata kuwahamasisha wananchi wetu waweze kuitikiwa wito wa kulima zao ambalo halina soko, lakini nilikuwa nataka nitoe ushauri ufuatao ili haya yote yaendane kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza watu wa Wizara ya Kilimo lazima watueleze idara zao zinazohusiana na utafiti zinafanya kazi gani, idara zao zinazohusika na suala la kutafuta masoko zinafanya kazi gani? Kama tulijua India watavunja mkataba wa kununua mbaazi kwa nini hawakutuambia? Na sheria au hatua gani zimechukuliwa pale mkataba unapovunjwa katikati? Ni harasa kiasi gani ambayo wakulima wetu wameipata kwa kuweka mazao yao ya mbaazi ghalani bila kununuliwa mpaka sasa hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba ushauri au kumtaka Mheshimiwa Waziri wa Kilimo aseme kwa msimu ujao tuna sababu ya kulima mbaazi? Kama tunakiwa tulime, tulime tani ngapi na tutazipeleka wapi? Vinginevyo hatutakwenda kuwashawishi tena wakulima wetu walime zao ambalo halina faida badala yake ni bora tukaelekeza nguvu kulima kitu ambacho kitaenda kuwasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nilizungumzie ni eneo la zao la muhogo, Wachina wameshaingia mkataba wa kutaka muhogo kutoka nchi ya Tanzani. Moja maeneo ambayo tunalima mihogo kwa wingi na miogo bora ni pamoja na Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Nachingwea. Ni vizuri sasa tunapojadili habari ya viwanda lazima tuseme tuna mkakati gani wa kweli kujenga kiwanda kitakachoshughulika na suala nzima la ununuzi wa mihogo na usindikaji wa mihogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi nikiangalia kablasha zote sijaona sehemu yoyote ambako tunaelekezwa au kuna maelekezo ambayo yataonesha nia thabiti ya Serikali katika kwenda kuwekeza ili wakulima wetu wapate sasa mazao mbadala badala ya kung’ang’ania kulima mbaazi ambazo tume-fail basi nizuri tukaelekeza nguvu katika mazao kama korosho pamoja na mihogo ambayo tunafikiri itatuletea tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie eneo ambalo linaenda sambamba na viwanda. Huwezi kujadili viwanda, huwezi kujadili uzalishaji wowote kama hatuwezi upatikanaji wa nishati ya uhakika. Bado Mkoa wa Lindi Wilaya ya Nachingwea na maeneo yote yanayozunguka kanda nzima tatizo la umeme limekuwa ni kiwazo kikubwa sana. Leo wananchi wetu hawatuelewi sisi wawakilishi wao, wananchi wetu hawaielewi Serikali inafanya nini ikiwa bado wananchi mpaka sasa hivi tunawahamasisha wafanye shughuli za kiuchumi lakini hawana umeme ambao zitawasaidia kufanya shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa heshima na taadhima, tunatambua kazi inayofanyika na sisi tunathamini, lakini ni muhimu sasa tukalichukua hili kama jambo la dharura. Tumeaidiwa sana kwamba mitambo itafungwa mashine zitanunuliwa; gesi inatoka kwetu lakini bado Mikoa ya Lindi na Mtwara mpaka sasa hivi hali ni mbaya hali ya uchumi inadidimia kwa sababu hakuna umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, kama tatizo ni fedha tunaomba utupatie fedha au uwape watu wa Wizara fedha au uwape watu wa Wizara ya fedha waweze kwenda kurekebisha upatikanaji wa umeme ili wananchi waweze kuzalisha na waweze kufanya shughuli za kiuchumi. Sasa hivi hakuna shughuli inayofanyika ukienda katika maeneo yale, ndani ya dakika mbili umeme unakatika, imekuwa ni kero na ni imekuwa hadha kubwa sana kwa shughuli za maendeleo. Kila Mbunge atakae simama anayetoka kwenye maeneo hayo lazima atazunguza hoja ya umeme. Tunaomba sasa ifike wakati Mheshimiwa Waziri mipango tuayoipanga kikanda ni lazima sasa tuelekeze mambo muhimu ikiwemo hili eneo la nishati ambalo sisi tunafikiri kwetu ni jambo la msingi na ni jambo ambalo litatusaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kujadili viwanda, huwezi kujadili uchumi kama huna mawasiliano ya uhakika na yaliyo safi. Serikali imefanya kazi kubwa mimi natambua, kwa mwaka wa jana na mwaka wa juzi mpaka kufika sasa hivi ziko ahadi ambazo tayari zimeshaanza kutolewa na nina hakika zitatekelezwa. Hata hivyo naomba Mheshimiwa Waziri katika mipango uliyoipanga, ziko barabara za kimkakati na za kiuchumi ambazo huwezi kujadili maendeleo ya nchi hii ukaziacha barabara hizo bila kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunajadili namna ya kuunganisha barabara za Wilayani kwetu, barabara ya kutoka Nachingwea - Masasi, Nachingwea - Nanganga kwa muda mrefu tumehaidiwa kupata fedha lakini bado utekelezaji haujaanza. Kwa mara ya mwisho tayari tumeshaambiwa wakandarasi wamepatikana bado kupitisha tenda kwa ajili ya kwenda kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri jambo hili ni la msingi sana. Leo hii tunatoa tani kwa tani za korosho kutoka Nachingwea kupeleka Mtwara kupeleka Lindi, hakuna sehemu ambako tunazipitisha na zile korosho zikafika kwa usalama. Magari mengi yameacha kufanya kazi kwa sababu barabara ni mbovu. Ni fedha kiasi gani tunapoteza kwa sababu ya ubovu wa barabara? Tunaomba ahadi ya kutengenezewa kwa kiwango cha lami na bahati nzuri matamko ya viongozi wetu yameshatolewa, tunaomba utekelezaji uanze katika mwaka huu wa fedha kwa wale wakandarasi ambao wameshapewa hii kazi. Hapa muhimu ni kupata fedha kwa ajili ya kuanza kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha tulichangiwa au tuliele…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wametoa pongezi kwa Serikali kwa kazi nzuri ambayo wameifanya na wanaendelea kuifanya. Vilevile naomba nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uwasilishaji wa hotuba yake. Watanzania wanaona, Watanzania wana akili, lakini ambacho wenzetu walikuwa wanakililia na ndicho ambacho Mwenyezi Mungu ametujaalia, sisi tunaendelea kumuombea Mheshimiwa Magufuli kwa kazi nzuri ambayo anaifanya ya kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote ndugu zetu wa upande wa pili walitaka Mheshimiwa Rais ambaye atathubutu, Rais ambaye atakwenda kutenda, kwa hakika Mheshimiwa Magufuli anatenda na sisi Wabunge wake tuko nyuma yake tunawa-support Waheshimiwa Mawaziri wetu kwa kazi nzuri ambayo wanaifabnya ya kuwatumikia Watanzania na hatimaye naamini Watanzania wale wale watakwenda kufanya maamuzi mwaka 2020 kwa kadri wanavyoendelewa kutumikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi naomba nichukue nafasi hii kutoa ushauri; yako baadhi ya maeneo ambayo kwenye bajeti ya mwaka jana nilisimama hapa nilishauri, lakini niishukuru Serikali yangu kwa sababu baadhi ya mambo mengi wameyafanyia kazi na kwa wakulima wetu sisi ambao tunawawakilisha yameanza kuleta tija kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge waliotangulia wa Mikoa ya Lindi na Mtwara wamezungumzia sana masuala ya elimu, kilimo, miundombinu, nishati na maeneo yote yanayohusu huduma za kijamii. Mimi naomba nijielekeze kwenye eneo la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulitoa mapendekezo ya kusaidiwa wakulima wetu kupata pembejeo hasa sulphur bure na Serikali yetu sikivu ilifanya hilo zoezi kwa kutoa sulphur na pembejeo nyingine kwa wakulima wetu. Uzalishaji ulipanda na wakulima wetu wamepata tija kubwa sana kwa zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na kutoa hizi sulphur na pembejeo nyingine bure bado yako maeneo ambayo tulifikiri ni muhimu tukaendelea kushauri, tukamshauri Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Wizara ya Kilimo waangalie namna ambavyo wanaweza sasa ku-fast track ili wakulima wa maeneo haya waweze kupata pembejeo kwa haraka iwezekanavyo. Hapa tunapozungumza leo ni mwezi wa nne tayari watu wameshaanza maandalizi ya mikorosho. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba sana watu wa Wizara ya Kilimo waharakishe upatikanaji wa pembejeo ili wakulima wetu waweze kuhudumia mikorosho yao kwa wakati ili waweze kuendelea kuzalisha na hatimaye tuliingizie taifa letu kipato kikubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka pia nishauri ni eneo ambalo linahusu malipo. Utaratibu ambao umetumika kwa msimu wa mwaka jana 2017 toka tumeanza utaratibu huu mpya wa stakabadhi ghalani ulioboreshwa bado kuna baadhi ya makampuni ambayo yamekuwa yanachukua korosho za wakulima yameendelea kuchelewesha malipo kwa wakulima wetu. Yako baadhi ya maeneo mpaka sasa hivi baadhi ya makampuni hawajamaliza kulipa fedha za wakulima ambazo zimeshauzwa toka mwaka jana wakati ambapo minada ilishafungwa toka mwezi wa kumi na mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo pamoja na timu yake watie mkono katika kuhakikisha makampuni yote ambayo yalichukua korosho za wakulima wanamalizia kulipa malipo ili wakulima waweze kupata nafasi ya kuhudumia mashamba yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nilishauri Serikali yetu ni eneo la ufufuaji wa viwanda. Katika jimbo la Nachingwea tunacho Kiwanda cha Ubanguaji wa Korosho ambacho kwa muda mrefu hakifanyi kazi. Pia kupitia Wizara yetu ya Viwanda ambayo tayari nilishakwenda kufuatilia walitupa maelekezo ya kufufuliwa kwa viwanda vyote ambavyo vilishakufa tangu muda mrefu. Korosho inayozalishwa katika maeneo haya tulipenda sana ipate thamani kubwa zaidi kwa kubanguliwa katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wawekezaji ambao wameingia ubia na baadhi ya vyama vyetu vikuu ikiwemo Lindi Farmers. Hata hivyo bado uwekezaji ambao unaendelea kule haujakaa vizuri, kupitai Wizara ya Viwanda Mheshimiwa Waziri lakini pia watu wa kilimo naomba watie mkono waone wale wawekezaji wa Sunshine ambao wamechukua viwanda vya Nachingwea, Mtama pale pamoja na maeneo mengine ya Newala waweze kuona nini ambacho kinaendelea ili ikiwezekana katika msimu huu wakulima wetu waweze kubangua korosho na kuipandisha thamani ili tuweze kupata pesa kubwa zaidi ya hii ambayo tunaipata sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nilishauri ni eneo la stakabadhi ghalani katika mazao mengine. Tunakwenda kwenye msimu wa kilimo cha ufuta Mkoa wa Lindi tumeadhimia kuingiza ufuta safari hii katika stabadhi ghalani. Niombe Wizara ya Kilimo ione namna inavyoweza kuhamasisha na kuangalia mikoa mingine yote inayolima ufuta ili tutakapoanza kwenda kutekeleza mfumo huu basi ukae katika misingi ambayo itakuwa haitoleta shida na haitopishana kati ya mkoa mmoja na mkoa mwingine; na hii kwa sababu kipindi cha nyuma ufuta umeuzwa kwa kila mkoa kwa utaratibu ambao si ule ambao tumeuzoea wa stakabadhi ghalani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tulishakuja kwako mwaka jana na mwaka huu sisi tumeshapitisha katika vikao vyote tulikuwa tunafikiri ni wakati wenu sasa kama Wizara muone namna ambavyo mtasimamia ili tuhakikishe mfumo huu utakapoanza kwa msimu huu basi uwe ni uniform katika maeneo yote yanayolima ufuta, lengo likiwa ni lilelile kuongeza tija kama ambavyo tunafanya vizuri katika zao la ufuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitajka nilkizungumzie ni eneo la zao la mbaazi. Mwaka jana tumelalamika sana juu ya changamoto za bei kwa zao la mbaazi ambalo wakulima wetu wengi wamechangamkia na kuiona fursa. Mheshimwa Waziri wakati anakuja hapa tulimuomba atupe ufafanuzi, lakini pia atueleze namna ambavyo wale wanunuzi hasa Wahindi ambao waliingia mkataba walivyojipanga kwenda kununua mbaazi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunapata shida kidogo kuwahamasisha wakulima wetu juu la suala la ulimaji wa mbaazi kwa sababu bado hatujawa na uhakika. Kipo kitengo ambacho kinashughulika na utafiti ndani ya Wizara ya kilimo, tunaomba kitengo hiki sasa kitoe maelekezo; kitoe dira lakini pia watupe uhakika wa masoko ili tuweze kupata nguvu ya kuwahamasisha wakulima wetu kama wanaweza wakaendelea kulima mbaazi kama zao la biashara au walime kama zao la chakula kama ambavyo tulikuwa tunafanya kipindi cha nyuma. Jambo hili nafikiri litatusaidia ili kuweza kuondokana na kile ambacho kimejitokeza miaka miwili mfululizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pilli ambalo nilitaka nichangie ni suala zima la miundombinu ya barabara. Hatuwezi kujadili maendeleo hatuwezi kupanga mikakati mizuri kama hatuwezi kuangalia hali ya barabara zetu. Kwa mwaka jana barabara ya Masasi - Nachingwea - Nanganga, tulitengewa shilingi bilioni tatu na milioni mia tano; nimefuatilia sana na ninaendelea kufuatilia sana. Hiki ni kilio cha wanachi wa jimbo la Nachingwea ambao wanapakana na Wilaya ya Masasi, wanapakana na Wilaya ya Ruangwa, Liwale. Barabara hii ni barabara ya kiuchumi; naomba niwaombe watu wa Wizara ya Ujenzi ya waone namna wanavyoweza kwenda kuanza utekelezaji wa ahadi ambayo wamenihaidi kwa miaka miwili sasa mfululizo; kwamba ujenzi utaanza na anatafutwa mkandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa jimbo la Nachingwea na maeneo yote ya jirani wamenituma na wanaendelea kunisisitiza kuendelea kuiomba Serikali yao sikivu iweze kuanza ujenzi huu kwanza kwa kulipa fidia, lakini pili kwa kuanzisha ujenzi ambao sasa utatusaidia kusafirisha mazao yetu bila matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiondoa barabara hii iko barabara inayotoka Nanganga kwenda Ruangwa kwenda kutokea Nachingwea barabara hii tayari usanifu umeshafanyika tunasubiri ahadi ya kuanza utekelezaji wa ujenzi wa kiwango cha lami. Iko barabara inayotoka Nachingwea kwenda Ruangwa kuunganisha Kiranjeranje; ni barabara ambayo ikifunguliwa nayo itakwenda kufungua uchumi wa Mkoa mzima wa Lindi kwa sababu Wilaya ya Nachingwea na Wilaya za jirani ndizo Wilaya ambazo zinaongoza kwa kusafirisha na kutoa mazao ambayo kimsingi yanaletea faida kubwa sana taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia ni eneo la nishati. Hali ya upatikanaji wa umeme katika mikoa yetu si mzuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzunguzaji)

MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba sana kupitia watu wa Wizara mashine walizozileta Lindi waende wakazifunge, muda tuliokaa kusubiri unatosha sana. Tumepewa miezi minne umeme utakwenda kutatuliwa, lakini muda huo ni mwingi tunaomba Wizara wazifunge zile mashine ambazo tayari wameshazileta ili tukae tuwe na umeme wa uhakika ambao utatuwezesha kuzalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nikushukuru sana na ninaomba nionge mkono hoja kwa asilimia mia moja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya Waziri wa Ujenzi. Kazi inafanyika na naomba niungane na wenzangu waliotangulia kutoa neno la kushukuru kwa kazi ambazo zinaendelea kufanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo kimsingi ambayo niliomba nichangie ili kuweza kuona namna ambavyo watu wa Wizara ya Ujenzi wanavyoweza kuendelea kusukuma baadhi ya kazi ambazo tayari zimeshaanza na zimeshaanzishiwa utaratibu wa kukamilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo nataka nilizungumze ni kuhusu suala la barabara ya Masasi kwenda Nachingwea. Barabara hii nikisoma katika ukurasa wa 148 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, wameeleza na wameonesha kiasi cha fedha ambacho wamekitenga jumla ya bilioni tano na hii ni nyongeza ya fedha shilingi bilioni moja na milioni 500 kutoka ile bajeti ambayo wamei-carry forward kutoka bajeti ambayo tumeimaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Nachingwea, Masasi na maeneo yote ambayo wananufaika na barabara hii, naomba nitoe neno kwa sababu ni hatua kubwa ambayo kimsingi tumeipigania kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia iko barabara ambayo inatoka Nanganga kwenda Ruangwa na inaenda kuunganisha na Wilaya ya Nachingwea. Nayo pia nimeona katika ukurasa huo huo wa 148 na ukurasa wa 208 imetengewa shilingi bilioni tano pia kwa maana fedha hii ikipatikana utaratibu wa kuanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami utafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeona milioni 800 katika kuanza utaratibu wa kufanya feasibility study kutoka Nachingwea kwenda Liwale. Haya yote ni mambo ambayo kimsingi mwanzo hatukuwa nayo, lakini Wizara wameonesha kwamba sasa wanayo nia ya kuanza kufanyia kazi barabara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kusema hayo, nimwombe sana Mheshimiwa Profesa Mbarawa, nimekuwa na yeye, nimekuwa nafuatilia kwake kwa karibu sana juu ya umuhimu wa kuanza kujengwa kwa hizi barabara. Ni muda mrefu sasa tumeahidiwa kwamba anatafutwa mkandarasi ambaye ataanza kufanya kazi, lakini mpaka sasa hivi kazi bado haijaanzwa na nimeendelea kufuatilia kupitia Wizarani kuona ni lini kazi hii na fedha hii ambayo tumetengewa itaenda kufanya kazi ili tuweze kutatua changamoto ya barabara ambayo kimsingi tumeipigia kelele kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii pamoja na kwamba ni ya muda mrefu ya kutoka Masasi kwenda Nachingwea barabara hii bado taratibu na speed yake kidogo inatutia mashaka sisi ambayo tayari tumeshawaelekeza wananchi wetu kwa majibu ambayo tumepewa kwamba itaanza kujengwa. Kwa hiyo, kupitia hotuba ambayo utakwenda kuhitimisha Mheshimiwa Profesa Mbarawa tunaomba atupe maelezo na haya ni maelezo ambayo wananchi wa Jimbo wanapenda kuyafahamu. Ni lini hii barabara hasa itaanza kwenda kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu ni ahadi ambayo kimsingi sasa ni kama tayari watu imeshaanza kuwachosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kidogo nipate ufafanuzi kuhusu barabara hii ya Nachingwea kwenda Masasi, ilikuwa inasomeka ni barabara ya Nachingwea - Masasi - Nanganga, lakini nikisoma kwenye hii hotuba barabara hii sasa naona kama kuna kitu kinaondolewa. Jumla ya barabara hii kwa bajeti ya mwaka jana ambayo walitupitishia ilikuwa inasomeka kilometa 91, lakini sasa hivi kuna kilometa 41 ya kutoka Masasi kwenda Nachingwea tu, Nanganga haizungumzwi na sasa hivi tunaizungumza barabara ya kutoka Ruangwa - Nanganga - Nachingwea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii ya katikati sijajua nini kimetokea hapo kwa sababu hii yote ni barabara moja. Ningependa kuwakumbusha watu wa Wizara, kama wamesahau basi ni vizuri tukarekebisha hili jambo kwa sababu tayari linatupa shida kutoa tafsiri sahihi ya barabara hii kama ambavyo tulianza ule mchakato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naomba pia nichukue nafasi hii kuwakumbusha watu wa Wizara ya Ujenzi, pamoja na kuunganisha hizi barabara ambazo nimezitaja, bado tunaona umuhimu wa kutengenezewa barabara ya kutoka Nachingwea kupitia Ruangwa Mjini kwenda Namichiga kwenda kutokea Kiranjeranje. Barabara hii ina urefu wa takriban kilometa 107.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana, barabara hii ndiyo itakayounganisha watu wanaotoka Tunduru, watapita Masasi, wanakwenda Nachingwea, wanatokea Ruangwa wanaenda kutokea Kiranjeranje, tayari kwa kwenda Dar es Salaam, hakutakuwa na sababu ya kupita Lindi Mjini na maeneo yale ambayo kimsingi tutakuwa tumepunguza umbali mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii sisi katika ngazi ya mkoa tayari tumeshaizungumza na tumeshaipitisha. Kwa hiyo, tunaomba watu wa Wizara katika bajeti yao wakumbuke kwamba kuna hii barabara na bado ni barabara muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingine ambayo ningependa pia kuwaomba watu wa Wizara na Mheshimiwa Kwandikwa tulishazungumza juu ya hii barabara na mwenyewe ameshafika, amefanya ziara katika wilaya yetu ya Nachingwea. Tunayo barabara ya kutoka Nachingwea kwenda Kilimarondo kutokea Lumesule. Kwa ngazi ya Mkoa kupitia TANROADS tayari tumeshafanya taratibu zote za kuipandisha hadhi. Tulichokuwa tunaomba katika mipango ya Wizara, barabara hii iingizwe katika utaratibu wa kufanyiwa kazi ili tuweze kufungua mawasiliano kati ya Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka nizungumzie ni eneo la mawasiliano. Mheshimiwa Nditiye nimekwenda sana kwake, lakini pia naomba nimwombe, kazi niliyomfanyia nikiwa Kibondo nami pia naomba alipe fadhila awafanyie kazi watu wa Nachingwea. Tarafa ya Kilimarondo ambayo inajumuisha Kata za Kiegei, Matekwe, Mbondo, hizi kata kwa muda mrefu hazina mawasiliano ya mtandao wa simu, nimeshapeleka haya majina kwako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana ndugu yangu, kaka yangu, watu hawa wameteseka kwa muda mrefu sana wanahitaji mawasiliano. Sasa hivi wanatumia TTCL tu na TTCL hii toka mwezi wa 12 mpaka sasa hivi mawasiliano bado wananchi wale kule wanatumia message tu simu hazitoki. Tunaomba atusaidie katika Mfuko huu wa Fursa sawa wa Mawasiliano, aweze kututengea utaratibu wa kuweza kupata mawasiliano na kampuni nyingine ili tuweze kuwaunganisha hawa watu wa tarafa pamoja na wilaya nzima ya Nachingwea ili tuweze kuboresha uchumi wa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia ni eneo la hawa wenzetu wa TARURA. TARURA wamefanya upembuzi yakinifu juu ya ukarabati wa barabara zinazozunguka Jimbo la Nachingwea. Kwa Mwaka wa Fedha uliopita waliomba bajeti ya bilioni moja karibu na milioni 300, lakini fedha ambayo ilitoka ni almost bilioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bilioni moja hii, milioni 750 imetumika tu kwa ajili ya kulipa madeni ya Mwaka wa Fedha uliopita. Fedha iliyobaki milioni 300 ndiyo ambayo imetumika kutengeneza barabara na itakayotumika, kitu ambacho bado kwa mtandao wa barabara wa Wilaya ya Nachingwea, fedha hii ni ndogo sana na umuhimu wa Wilaya ya Nachingwea unafahamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Nachingwea sasa hivi tunazalisha korosho, ndani ya Mkoa wa Lindi ndiyo tunaongoza, lakini mtandao wa barabara ni mbovu na hauwezi kuhimili taratibu zozote za kuweza kusafirisha mazao kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namwomba sana Mheshimiwa Waziri katika utaratibu wa fedha ambao wanaenda kuugawa, katika bajeti ya fedha ambayo wameitoa pamoja na kutoa ceiling ya mwaka uliopita, tumeomba jumla ya bilioni tatu, lakini mpaka sasa hivi kiasi ambacho wame-approve bado Wilaya ya Nachingwea hawajatoa hata shilingi moja. Tunashindwa kujua dhamira yao hasa ni nini katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio lazima Wabunge wote tukisimama hapa tuongee kwa kutokwa mapovu, tunaona umuhimu wa kuzungumza kwa lugha laini ili tuweze kuelewana kwamba keki ya Taifa hili tugawane katika misingi ambayo inalingana. Haipendezi kuona maeneo mengine wanapata fedha, barabara zao hazina umuhimu mkubwa sana, lakini maeneo mengine barabara zao hazipati fedha kama ambavyo sisi tumekuwa tunalilia. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atueleze anatupatia shilingi ngapi kwa ajili ya kukarabati barabara ndani ya Jimbo la Nachingwea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza jioni hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipitia na kuisoma vizuri hotuba ya Mheshimiwa Waziri na maombi ya fedha ambayo anaomba. Pamoja na yote ambayo yamewasilishwa nina mambo kadhaa ambayo napenda kwa niaba ya wananchi ambao tunawawakilisha hapa Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atupatie maelezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni uendelezaji wa zao la korosho. Ziko jitihada kubwa sana ambazo zimefanywa na Serikali yetu lakini pia iko kazi kubwa sana ambayo sisi Wabunge pamoja na Serikali tumeifanya katika kutoa tozo zile ambazo zilikuwa kandamizi kwa wakulima wetu na hii imepelekea angalau kuona tija kidogo. Hata hivyo, yako mambo ambayo naona ni busara sasa tuweze kuelekezana na pia tupeane ufafanuzi ili tuweze kuona namna bora ambavyo tutaliendeleza zao hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na Mfuko wa Pembejeo ambao kazi yake kubwa ilikuwa ni kuendeleza zao la korosho. Kwa msimu wa 2016/2017, ziko fedha nyingi sana (export levy) ambazo wakulima wa korosho wamekatwa. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kusimama atueleze kwa mwaka nilioutaja 2016/2017 ni kiasi gani cha fedha zao la korosho limechangia lakini pia Serikali itueleze ni kiasi gani imerejesha kwa ajili ya uendelezaji wa zao hili la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena Mheshimiwa Tizeba kila Mbunge aliyesimama kutoka Mkoa wa Lindi na Mtwara jambo hili amelizungumzia na mimi naomba kwa heshima na taadhima utakapokuja kusimama utuambie fedha ya export levy ambayo tulipaswa turudishiwe kwa ajili ya kununua pembejeo mpaka sasa hivi tunavyozungumza iko wapi na imetumika kufanya kazi gani? Kwa sababu utaratibu ambao sasa hivi unaendelea ni kinyume na makubaliano yetu ya awali na namna hata mfuko unavyotaka katika uendelezaji wa zao letu la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo pia naomba ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri ni nia haswa ambayo wenzetu wa Wizara wameanza kuionyesha. Kabla sijasema naomba kidogo niwakumbushe wale waliosoma historia. Kipindi cha ukoloni nchi hii iligawanywa katika kanda, yako maeneo ambayo yalikuwa yanalima mazao kutokana na hali ya hewa jinsi ilivyo. Leo hii ukienda Mwanza utakuta pamba, Kusini mwa Tanzania utakuta korosho na ndiko inakostawi na ndiko inakotoka korosho bora na ukienda Kaskazini huko utapata kahawa na chai. Leo hii sijajua ni tamaa kiasi gani imetuingia tunataka tulihamishe zao la korosho kutoka Kusini ambako lilikuwa linalimwa tulifanye kuwa zao la Tanzania nzima. Siyo jambo baya, kama tumeamua kuweka mkakati huo basi si vibaya Mheshimiwa Waziri atuambie ni kiasi gani cha fedha ya kahawa anaenda kutuletea watu wa Lindi na Mtwara ili na sisi tukaanze kulima mazao haya ya biashara ambayo yatakwenda kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki kinachofanyika nafahamu kina nia njema kwa wakulima na Watanzania na hii ni kwa sababu tayari tumeshaanza kuona faida kubwa ambayo inapatikana kwenye zao la korosho. Ukichukua mathalani Dodoma leo hii tunakuja kupanda korosho, mikorosho ambayo mmeisambaza mwaka uliopita mpaka sasa hivi iko majumbani inakauka tu, hamna mtu yeyote ambaye anaishughulikia na anaifanyia kazi. Wakati mikorosho hii tungeweza kuisambaza Tandahimba, Mauta, Nachingwea na Liwale ambako hali ya hewa inaruhusu ingeweza kuleta tija zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba Mheshimiwa Waziri atuambie hasa anachokusudia kukifanya ni nini. Kama lengo ni kutawanya keki hii basi si vibaya na sisi watuletee fedha za pamba, kahawa na chai ili na sisi tuweze kulima katika maeneo yetu kwa sababu ardhi yetu nayo pia inaweza kuhimili na kupokea mazao hayo kama ambavyo maeneo mengine wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kupata ufafanuzi kupitia watu wa Wizara. Ukisoma Ripoti ya CAG, ukurasa wa 148 – 151, umeeleza ubadhirifu mkubwa sana ambao umejitokeza katika uzalishaji wa zao la korosho. Ziko hatua ambazo tulitamani kuziona zinachukuliwa na zitatusaidia sana kuendeleza zao la korosho kama ambavyo Serikali na watu wa Wizara wamekusudia. Najua uko wakati ambao tutajadili ripoti ya CAG lakini ni vizuri wakati tunaenda kujadili bajeti ya Wizara hii lazima tuone hatua na dhamira gani watu wa Wizara wamekuwa nazo kwa ajili ya kuhakikisha ubadhirifu ambao umeendelea kujitokeza kwenye zao la korosho unadhibitiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ukisoma utaona kupitia Mfuko wa Hisani wa Kuendeleza Zao la Korosho iko fedha ambayo ilipaswa tayari iwe imeshakatwa kutoka kwa watu wa vyama Sh.4,085,000,000. Mpaka mwaka huu wa fedha ambao tunaenda kuumaliza fedha hii haieleweki ipo kwa watu wa vyama vya ushirika kwa maana kwenye akaunti zao au ilitakiwa iwe wapi kwa sababu wako watu ambao wamekatwa na hawa ni wakulima ambao sisi tunawawakilisha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba sana, haya siyo maneno yangu ni ripoti ya CAG ukiisoma vizuri inabainisha na inataka watu wanaohusika na eneo hili watueleze fedha hii shilingi bilioni 4 iko wapi mpaka sasa hivi ili tuweze kuwarudishia wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine katika ripoti hii ya CAG ukiiangalia vizuri utaona wako watu ambao wamepewa fedha kwa ajili ya ubanguaji wa korosho. Iko Kampuni moja inaitwa Jumbo Cashewnuts na kikundi cha akina mama wanaonekana wamechukua fedha zaidi ya shilingi milioni 500, fedha hii haijarejeshwa mpaka leo tunavyozungumza. Wako viongozi wa Bodi ya Korosho wamechukuliwa hatua lakini hatuamini kwamba wale wachache waliochukuliwa hatua ndiyo pekee ambao wamehusika na upotevu wa fedha za wakulima. Tunaomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na timu yake watuambie wote wanaowasaidia viongozi wote wa Bodi ya Korosho ni hatua gani watakwenda kuchukuliwa kwa usumbufu na hasara kubwa ambayo wamewasababishia wakulima wetu ambao kimsingi mpaka sasa uendelezaji wake unasuasua. Wale wanaopaswa kukopeshwa hizi fedha bado hawajakopeshwa kwa sababu tu kuna watu ambao makampuni yao yamechukua fedha na hawajazirejesha kwa wakulima ili tuweze kuingiza katika mzunguko ambao utatusaidia kuwakomboa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nilizungumze ni suala zima la uchelewaji wa malipo. Yako makampuni leo tunazungumza mwezi wa tano takribani miezi sita imepita toka tumefunga minada bado hawajalipa wakulima fedha zao. Hili ni jambo la hatari na la kukatisha tamaa sana. Wakulima wetu walio wengi sasa hivi wanapata shida ya kuendesha maisha yao kwa sababu fedha zao kuna makampuni wamezikalia. Ziko sheria ambazo zinataka wale waliochukua fedha hizi kuchukuliwa hatua lakini mpaka sasa hivi kesi nyingi ziko polisi na wakulima wanaopaswa kulipwa hawajalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri alishafika katika maeneo yetu na hasa aliishia Masasi lakini naomba niwape taarifa, walichokiona Masasi ni sehemu tu bado maeneo ya Nachingwea ukienda Liwale kuna wananchi mpaka leo napozungumza, mkihitaji ushahidi wa haya nitakuja niwaambie hawajalipwa fedha zao na wanaendelea kuzungushwa. Kesi zinaenda polisi hazifikishwi Mahakamani, hatujui sababu za kesi hizi kutofikishwa Mahakamani ni nini wakati wakulima walishatoa korosho zao kwenye makampuni haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauri makampuni yanayoshindwa kulipa yaondolewe katika ununuzi wa korosho za wakulima. Jambo hili huu sasa mwaka wa pili halijafanyika na makampuni haya yanaendelea kushiriki kwenye ununuzi wa korosho. Sasa hii kidogo inatupa shida kujua dhamira yetu haswa ipo katika eneo gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nichangie ni zao la mbaazi. Mheshimiwa Waziri Mzee Tizeba kila tunaposimama hapa tunazungumza suala la mbaazi, uchungu wake ni kama bado haujawafikia lakini kwa sisi tunaokaa na hawa wakulima hili jambo tutapaza sauti kila tutakapopata nafasi ya kusimama hapa mpaka Serikali itakaposhtuka. Wakulima wetu bado wanaendelea kuzalisha mbaazi lakini hakuna mikakati yoyote ambayo itaenda kumkomboa mkulima anayelima mbaazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako majibu hapa tumepewa kwamba tulime mbaazi na ikiwezekana tule kama mboga haina shida, hizo sisi tunakula kama mboga lakini bado tunaomba majibu ya kina. Nimeisoma hotuba vizuri sana inaeleza kwamba Serikali itaendelea kuimarisha soko la ndani lakini pia itaendelea kuhamasisha viwanda ambavyo vitafunguliwa kwa ajili ya kuendeleza au kununua zao hili. Tunaomba kupitia Kitengo cha Utafiti watuambie bado tuna mahitaji ya mbaazi? Kama hatuna mahitaji tuwaambie wakulima wetu wasiingie hasara ya kulima mashamba makubwa ambayo tija yake mpaka sasa hivi bado haijaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha naomba jambo hili alipe kipaumbele, tunaomba statement, tunaomba kauli yake vinginevyo mwezi wa saba, wa nane tutakuja hapa kumlaumu kwamba kwa nini mbaazi haijanunuliwa wakati hili jambo siyo lake yeye.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya bajeti. Nami niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake kwa kutuletea yale mambo ambayo tunafikiri yana manufaa makubwa kwa wananchi wetu lakini kwa Taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, naomba nijielekeze kwenye eneo moja linalohusu kilimo. Kabla sijazungumza lolote, naomba nijaribu kumpitisha kidogo Mheshimiwa Waziri na timu yake ili waweze kujua wapi tumetoka. Toka mwaka 2015 wakati tunaingia hapa kwa mara ya kwanza tulitoa mapendekezo kadhaa kwa ajili ya kuboresha mazao yetu makubwa ambayo yamekuwa yanaliingizia Taifa letu kipato. Katika mazao haya lipo zao kubwa la korosho ambalo limekuwa linalimwa kwenye baadhi ya maeneo au kwenye baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada ambazo zimefanywa na Wizara ya Fedha kwa kutondoa tozo tano ambazo zilikuwa kikwazo zimepelekea kuongeza tija lakini pia kiasi kikubwa cha fedha katika mzunguko mzima, kwanza kwa wakulima wetu lakini pia kwa Taifa zima. Kama mwakilishi wa wananchi, nitakuwa mtovu wa fadhila kama sitatoa shukurani kwa sababu ni Mheshimiwa Mpango ndiye aliyefanya kazi ya kuondoa zile tozo za usafiri, unyaufu, kulipa wale viongozi wa vyama vikuu na maeneo yale yote ambayo nafikiri yalipelekea kwa mara ya kwanza kuanza kuuza korosho kwa bei kubwa na wananchi wameweza kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na kumpa pongezi hizi kidogo nimepata mashaka kupitia pendekezo la bajeti ambayo iko mbele yetu. Nilikuwa nasoma katika ukurasa wa 69 juu ya azma ya kuleta mabadiliko kwa ajili ya kuhakikisha fedha zinazotokana na mazao ambayo yako chini ya Bodi za Mazao kufikiria kuziingiza katika Mfuko Mkuu. Jambo hili Mheshimiwa Dkt. Mpango na Serikali yangu naomba niseme kwetu sisi kama wakulima hamtakuwa mmetusaidia kwa namna ambavyo mmefikiria. Nimwombe Mheshimiwa Dkt. Mpango wazo hili ambalo analileta hebu afikirie kuliondoa kwa sababu atakwenda kutugombanisha na wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hoja kwa nini nasema hivi lakini yako mapendekezo ambayo napenda kwa umakini ayachukue na akayafanyie kazi. Asipofanya hivyo, nafikiri jana amemsikia Mbunge mwenzetu mmoja alikuwa anazungumza kwa utani lakini alichokuwa anakizungumza ndicho kitu ambacho kipo kwa wakulima ambao wametutuma kuwepo hapa ndani. Sisi Wabunge ambao ni wenye Serikali hii tusingependa kuona jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali zinaenda kuharibika kwa ajili ya kufanya yale ambayo tunaona hayatatusaidia na wala hayatawasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya yale mapendekezo ambayo nataka kuyasema, Mheshimiwa Mbunge mwenzetu wa Mtama wiki mbili zilizopita alikuja hapa na hoja ambayo kimsingi iko pending mpaka leo na ilikuwa pending kwa sababu Mheshimiwa Dkt. Mpango wakati tunamuita kwenye kikao cha bajeti aje atuambie liko wapi rejesho la fedha za wakulima ambazo zinafika takribani bilioni 81 bahati mbaya sana hakutokea kwenye vile vikao. Sasa leo anapokuja na mapendekezo ya kutaka kuchukua asilimia 100 ya fedha yote ambayo kimsingi ukisoma hiyo Finance Act ya mwaka 2010 inaeleza asilimia 35 itaingia Hazina, asilimia 64 itarudi kwa ajili ya kuboresha zao hili la korosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la korosho linaboreshwa kwa kununua mbegu, mbegu hizi zinapandwa kwa maana ya miche, wako watu mpaka leo tunazungumza hawajalipwa fedha zao za kazi ambayo wamefanya ya ku-supply miche. Pia tunatakiwa tujenge maghala mpaka sasa hivi hatujajenga kwa sababu fedha haijarudi. Mbaya zaidi napozungumza leo wananchi wanagawana mifuko ya sulphur kitu ambacho siyo cha kawaida na kitakwenda kuondoa kabisa uzalishaji mkubwa ambao tumeufanya kwa miaka hii mitatu kutokana na mabadaliko tuliyoyafanya. Sasa ukifikiria kuchukua asilimia 100 ya fedha hii kutoka kwenye sheria hii ambayo nimeitaja, Mheshimiwa Dkt. Mpango anakwenda moja kwa moja kudidimiza na kuua zao la korosho. Pia nimhakikishie kwamba anaenda kuwagombanisha wananchi wa mikoa inayolima korosho pamoja na Chama chao cha Mapinduzi kitu ambacho tusingependa kitokee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunampenda sana Rais wetu na tunaamini Rais wetu anatupenda sana sisi wananchi na ndiyo maana alisikiliza kilio chetu, naomba Waziri asirudishe nyuma jitihada za Mheshimiwa Rais katika hili. Waziri akifanya hivi, hata mimi Mbunge wa CCM nakwenda kuungana na wananchi wangu kupinga hicho ambacho anakwenda kukifikiria kukifanya lakini tunakwenda kusimama na wakulima wetu moja kwa moja kuhakikisha maazimio haya ya kwenda kuchukua asilimia 100 ya fedha hii hayawezi kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nafikiri ni vizuri nikashauri na nimwombe Mheshimiwa Waziri kama nilivyomuomba kwanza aende kwenye takwimu. Bajeti tuliyomaliza au tunayomaliza 2016/2017 kwenye bajeti ya kilimo zaidi ya asilimia 10 tu ya fedha ambayo imeidhinishwa ilikwenda. Leo anaposema anaenda kuchukua asilimia 100 ya makusanyo ya korosho au ya mazao yote yaliyoko kwenye bodi na wakati asilimia 90 ya bajeti nzima haijaitekelezwa, ndiyo kusema kwamba hata hizi asilimia ambazo wanataka kuzichukua na kwamba zao hili litagharamiwa na Serikali Kuu tunaenda kufeli. Kwa sababu bajeti ya jumla peke yake tayari tumesha-prove failure, tumeshindwa kutoa fedha na hivyo leo kilimo tunachozungumza ambacho ndiyo uti wa mgongo wakulima wetu hawajaweza kunufaika nacho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Waziri kwamba zoezi la kwenda kuichukua hii fedha halitakuwa na tija kwa sababu hata hiyo bajeti kuu ya Wizara nzima tumeshindwa hata kufikia asilimia 50 ya utekelezaji wake. Tukichukua hii maana yake unaenda kuondoa moja kwa moja uzalishaji na unaenda kutudidimiza moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nilitaka pia nijaribu kumpitisha Mheshimiwa Waziri ni namna gani ambavyo ataenda kutueleza na ataenda kuwaeleza wakulima. Kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 2005/2006, 2006/2007, 2007/2008 tuna zaidi ya shilingi bilioni 201 imekwama katika Wizara yake. Hela hii haijarudishwa na mpaka sasa hivi tunavyozungumza shilingi bilioni 10 tu pekee yake ndiyo imetolewa, tena yenyewe imetolewa kama mkopo kutoka NMB, kama ni mkopo maana yake ni nini? Wananchi wetu wanapaswa kulipia riba ya mkopo huu wakati fedha yetu ya ruzuku ambayo yeye ameshaichukua hajaturudishia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo anapoenda kuleta mabadiliko ya sheria na kutaka tubadilishe ili fedha iende Mfuko Mkuu atueleze fedha yetu ya miaka mitatu iko wapi na inaenda kufanya nini? Inafutwa au ndiyo sisi wakulima tayari tumeshadhulumiwa? Kitu ambacho kwa kweli narudia kusema, tena nasema nikiwa na utulivu wa hali ya juu Mheshimiwa Dkt. Mpango asitulazimishe, asitake kututia majaribuni kati ya sisi na wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tuendelee kuwa watiifu kwa Taifa letu na kwa Rais wetu kwa sababu tunampenda na tunataka awatumikie wananchi. Katika hili Mheshimiwa Dkt. Mpango tunaomba sitisha mara moja zoezi la kwenda kuchukua fedha ya wakulima ambayo nyingine mpaka leo hujairudisha na majibu hujatoa leo unakuja na mapendekezo mengine ambayo kwetu sisi hayana tija na hayatatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la lingine ambalo nataka nilizungumzie ni kuona namna gani ambavyo mapungufu ambayo wao wameyaona kama Wizara juu ya hoja walizozitoa wakati wanajibu kwamba kuna matumizi mabaya kwenye Mfuko wa Uendelezaji wa Zao la Korosho lakini solution haiwezi kuwa kwenda kuufuta ule. Nafikiri solution ilikuwa ni kufanya maboresho. Fedha ambazo wamezizuia maelezo yanayotolewa ni kwamba kuna matumizi mabaya ya honorarium na matumizi mengine, sisi hatuna tatizo katika hilo na tutaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali kupinga matumizi mabaya yasiyokuwa na tija lakini hatuwezi kuzuia na kuua zao zima kwa ajili tu ya eneo moja ambalo tungeweza kulibana kwa maana ya kuwabana watu wa Bodi ya Korosho na wale watumishi ambao wanatumia fedha hii. Yale yanayohusu kununua miche, kufanya utafiti, leo Chuo cha Naliendele hakifanyi kazi yoyote, magonjwa yameanza kuvamia zao la korosho watu hawana fedha za kulipia kwa sababu fedha yote imeingia kwenye Mfuko Mkuu na hairudishwi. Sheria ambayo imetungwa ni ambayo sisi kama Wabunge tunapaswa kuisimamia na tunapaswa pia kuiheshimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana lakini nimwombe Mheshimiwa Waziri Mpango hebu hapa tunapokwenda kuhitimisha zoezi hili binafsi sitamuunga mkono na naenda kupinga moja kwa moja wazo hili kwa niaba ya wananchi wangu ili tuhakikishe haki na hatima ya zao la korosho inaenda kuimarishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho atuambie, najua mapendekezo aliyoyatoa siyo kwa zao la korosho peke yake yako mazao mengine kama pamba, kahawa na mazao mengine. Hebu atoe takwimu ndani ya miaka mitatu kila zao ambalo amefikiria na lina bodi ni kwa kiasi gani mazao hayo yameingiza fedha katika Taifa letu? Kwenye kitabu chake kinaeleza pamba tumepata hasara, hapa anachoelekea kukifanya ni kwenda kuua pia zao la korosho ambalo linafanya vizuri kwa kisingizio cha kutaka kuchukua mazao ya Bodi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niseme siungi mkono hoja mpaka pale jambo hili litakapokwenda kukamilika, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuweza kuwa mchangiaji wa kwanza wa Mpango wa Serikali kwa mwaka 2019/2020. Naomba nijielekeze kwenye eneo moja baada ya kuwa nimeupitia mpango wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kabla sijasema nilichokusudia kusema naomba nitumie nafasi hii kwanza kupongeza jitihada kubwa ambazo zimekuwa zinafanywa na Serikali yetu katika kuhakikisha mipango tuliyoipanga mwaka 2018/2019 inakwenda, lakini wakati huo tuna-focus kuangalia namna ya kutekeleza mipango ya mwaka wa 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukamilisha mipango ambayo tunaipanga kwa sehemu kubwa lazima tuangalie mambo gani ambayo yanatuwezesha kuhakikisha mipango yetu tunayoipanga inakwenda sambamba. Leo naomba nijielekeze kwenye eneo moja tu la kilimo kwa sababu ya kazi kubwa au faida kubwa ambayo tunaipata kupitia kilimo ambacho tunakishiriki au tunakifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia kilimo ndiko ambako tumekuwa tunaboresha huduma nyingine za kijamii. Kupitia mipango ambayo Mheshimiwa Waziri leo ameiwasilisha hapa kwa sehemu kubwa ndiko ambako tunapata fedha kwa ajili ya kuhakikisha mambo mengine yote yanakwenda ikiwemo maji, afya, barabara, lakini pia tunapozungumzia viwanda lazima tuzungumzie malighafi ambazo zinatokana na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo naomba pia, nitumie nafasi hii kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Wamefanya kazi kubwa, lakini kwetu sisi wakulima ambao tunatokana na zao la korosho ambalo limetoa mchango mkubwa sana kwa mwaka wa fedha uliopita nimeona nilizungumzie hili kwa kina kwa sababu, kama sitafanya hivi hata wakulima ambao nawawakilisha hapa ndani nafikiri hawawezi kunielewa. Kwa hiyo, naomba nijielekeze zaidi kuzungumzia zao la korosho na namna ambavyo limeleta fedha nyingi kwa ajili ya kuimarisha uchumi wetu na hivyo kuhakikisha mipango tunayoipanga inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu wamefanya kazi ya kukaa na wanunuzi wa korosho, lakini pia, wamefanya intervention kubwa sana kuhakikisha hali inayoendelea sasa hivi katika maeneo yanayolima korosho haiendelei kuwa mbaya. Katika hili naomba nitoe pongezi kwa niaba ya wale ambao tunawawakilisha kwa sababu, walichokifanya viongozi hawa ni sehemu ya kilio ambacho sisi wakulima tayari tulishakuwanacho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ambazo zimechukuliwa na viongozi wetu bado yako mambo ambayo niliona nitumie nafasi hii kuishauri Serikali. Vikao walivyovifanya pamoja na wafanyabiashara, pamoja na kwamba, matarajio yetu yalikuwa ni kuona korosho za wakulima zinaondolewa, lakini bado mpaka leo ninapozungumza kwa makadirio ya haraka haraka kuna jumla ya tani 34,000 kupitia vyama vikubwa vitano mpaka sasa hivi zimekusanywa. Katika hizi tani ambazo zimekusanywa jumla ya tani 2,500 plus kwenda 3,500 ndizo ambazo zimeuzwa mpaka leo ninapozungumza kwa mnada uliofanyika leo kwenye baadhi ya maeneo ya Tandahimba kule kupitia TANECU.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii na muda ambao tunao kwa kweli, kidogo inatupa mashaka sisi wakulima ambao tumewekeza sehemu kubwa ya fedha zetu kwenye eneo hili. Kwa hiyo, nataka tuone kupitia watu wa Wizara ya Fedha, lakini pia kupitia watu wa Wizara ya Kilimo na pia kupitia Mheshimiwa Rais mwenyewe kwa sababu, yeye ndio mtu wa mwisho ametoa kauli na tunaamini kiitifaki yeye ndiye pia, anapaswa kurudi na kwenda kulizungumzia jambo hili, basi apokee mapendekezo ambayo yanatoka kwa wakulima ili tuweze kuwasaidia kuondokana na hasara ambayo inaweza kwenda kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara ambao walikaa kwenye kile kikao ni kama wamesusia, naweza nikasema hivyo. Kwa sababu, ukiangalia trend ya tani wanazozichukua na makubaliano yaliyofanyika hayafanani na kiasi cha korosho ambacho wakulima tunategemea tukiuze. Misimu kwa kawaida huwa inaanza mwezi wa 10, leo tunapozungumza ni mwezi wa 11, nimemsikiliza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo anazungumza kwamba, msimu wa korosho ni miezi mitatu, ni kweli, lakini kuna vitu ambavyo nafikiri bado hajaijua korosho na hajaiishi korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimueleze kwa sisi tunaotoka kwenye maeneo ya korosho, ikishaanza kunyesha mvua hiyo miezi mitatu ambayo anaihesabia ambayo mpaka sasa hivi hatujafanya biashara itakuwa tena hakuna biashara ambayo inaenda kufanyika kule mara mvua itakapokuwa imeanza kunyesha kutokana na Jiografia ya maeneo yetu, lakini pia kutokana na hali ya hewa ambayo inaathiri kwa kiasi kikubwa sana korosho za wakulima ambao wametumia gharama kubwa kuzihudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya juu katika minada hii ni Sh.3,016/= na bei ya chini imebaki Sh.3,000/= ileile, jambo ambalo sisi tunashukuru kwa sababu, Mheshimiwa Rais alizingatia gharama za uzalishaji ambazo wakulima wamezifanya katika kipindi chote cha kuandaa mashamba, kuvuna, kuokota pamoja na kupeleka kwenye maghala. Ushauri ambao nataka niutoe ni huu ufuatao; kwa sababu wanunuzi wameshindwa kununua hizi korosho kwa kadri ya makubaliano yalivyokuwa yamewekwa, pendekezo la kwanza ambalo nataka nitoe ni kwa Serikali kwa kadri ilivyokuwa imezungumzwa siku ile ya kikao ambacho Mheshimiwa Rais alifanya, Serikali ione uwezekano wa kuzinunua hizi korosho kama hiyo njia tumejipanga nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu ambayo nimeshaitaja kwamba, tuliotegemea wanunuzi wazinunue wameshindwa kununua na sasa hivi muda unakwenda na tunategemea watarudi kwenye duru ya pili ambayo pia, haioneshi matumaini ya kwamba, bei itaenda kupanda zaidi ya bei ambayo Mheshimiwa Rais ameipendekeza. Kwa hiyo, Serikali yetu kama imejipanga na fedha ipo, basi tunaomba ichukue hatua za makusudi za haraka kunusuru hali inayoendelea kule sasa hivi, ili korosho za wakulima ziweze kuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pendekezo la pili, hebu twende tuangalie kwenye Bodi ya Korosho yenyewe. Bodi ya Korosho kuna tozo na kuna fedha ambazo kama Serikali itaenda kuzikata nina hakika zitaenda kumpunguzia mnunuzi mzigo na hivyo azma ya kununua korosho kwa Sh.3,000/= itabaki palepale na haitaathiri pendekezo ambalo Mheshimiwa Rais amelitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tozo ya kwanza ambayo napendekeza ikatwe ni tozo ya service charge. Hawa wanakata Sh.10/=, badala ya Sh.10/=, nashauri Serikali ingewaagiza watu wa bodi wakate Sh.5/= ibaki kwa wanunuzi Sh.5/=, ibaki kwa watu wa bodi kwa ajili ya ku- service hizo huduma ambazo wanaendelea kuzifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la pili naomba nipendekeze kukata fedha ya kugunia; fedha ya gunia inakatwa Sh.52.5/= napendekeza ingekatwa Sh.42/= ili 10/= itakayokatwa iingie katika kuhakikisha mnunuzi habebi mzigo mzito kwa sababu wanazozitoa za kushuka kwa soko la dunia. Basi naamini kwa kufanya hivyo itaenda kupunguza uzito ule wanaoupata sasa hivi kwenda kununua korosho zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pendekezo la tatu tuiangalie pia, export levy ambayo kimsingi kuna 15% ambayo tayari hata Mheshimiwa Rais alishaizungumzia. Naomba nishauri hapa, badala ya 15%, Serikali ingebakiwa na 9% ili tuache 6% kwa wanunuzi, nayo pia itaenda kutusaidia. Ikiwezekana hii tutakwenda kusaidia kununua korosho kwa bei ambayo Mheshimiwa Rais ameipanga na hii nafikiri itaenda kutunufaisha sisi wakulima ambao tumeingia gharama kubwa kwa ajili ya kuhakikisha kilimo kinakwenda kutunufaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la mwisho katika eneo hili ni kupitia makato yale yote yaliyoko kwenye fedha ya mjengeko wa bei. Kuna makato ambayo kwa hali ilivyo na kwa sababu, hatukujipanga na hiki ambacho kinajitokeza, basi tungeangalia kwenye ile fedha ya mjengeko wa bei Sh.240/= kuna fedha kule za vyama, kuna fedha kule kwa ajili ya kuhudumia vyama vya ushirika, hizi zote tungeziangalia vizuri, lakini pia tungetoa maelekezo kwenye halmashauri zetu ziondoe zile fedha ambazo hazina ulazima kukaa kwenye fedha hii, ili mkulima aweze kunufaika, lakini pia, wafanyabiashara wasipate hasara ambayo wanafikiri wataipata kama watachukua korosho zetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Niungane na wenzangu waliochangia kwa kutoa pongezi kwa mawasilisho yaliyofanywa, lakini pia kwa upekee kabisa, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Wasaidizi wake wote ambao wanamsaidia majukumu ya kutekeleza mambo mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha tunawatumikia Watanzania ambao wametupa ridhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo bado pia naomba nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, takribani siku nne sasa amefanya ziara ndani ya maeneo ya Kanda ya Kusini. Wote mtakuwa mashahidi amefika Mkoa wa Mtwara na kwa muda mrefu sana, sisi wananchi tunaotoka katika ukanda huo tulikuwa na hamu kubwa sana ya kumwona Mheshimiwa Rais anakuja kule. Ujio wake kwetu umekwenda kutupa faraja kubwa sana, yako maelekezo mengi ambayo Mheshimiwa Rais ameyatoa kwa ajili ya kuhakikisha Watanzania wanapata zile huduma zote muhimu, lakini hapa kubwa ambalo ningependa nipongeze ni suala zima linalohusiana na korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, korosho kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ni sehemu ya uchumi wetu, ni sehemu ya maisha, lakini ni sehemu ya changamoto ambazo kwa wakati fulani kidogo tulipitia. Hata hivyo, kupitia ziara aliyoifanya ameenda kutuachia faraja kubwa sana na mimi kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nachingwea na kwa niaba ya wananchi ambao wanalima korosho tutakuwa watovu wa fadhila kama hatutathamini na kupongeza kile ambacho Mheshimiwa Rais amekielekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa sababu yeye ndiye msaidizi, tunaomba atufikishie salamu hizi kwa Mheshimiwa Rais na Watendaji wake wote wakiwemo Mawaziri wa Kilimo, ambao walichukua mawazo yetu na waliyafanyia kazi yale ambayo sisi tuliyashauri kwa niaba ya wananchi ambao wametupa nafasi ya kuwepo katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye ukurasa wa 27 mpaka 30 kwa sehemu kubwa wamezungumzia suala zima linalohusu kilimo. Ningependa nizungumzie zaidi kwenye eneo la kilimo kwenye namna bora ambayo tutakwenda kujipanga wakati tunaelekea kwenye msimu ujao hasa katika zao hili la korosho, ambalo ndilo hasa linalotuletea uchumi na ndilo ambalo hasa linatuletea kipato kama nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto tulizozipitia sehemu kubwa ili tuweze kuzirekebisha yako mambo ambayo ningependa nishauri kupitia hotuba ambayo imetolewa. Jambo la kwanza ni suala zima la kuhakikisha wakati tunajiandaa na msimu mpya wa 2019/2020, tuone namna gani ambavyo tunaweza kwenda kusambaza pembejeo za kutosha hasa sulfur pamoja viuatilifu vingine ambavyo tumekuwa tunavitumia katika kufanya uzalishaji. Jambo hili na kupitia Serikali yetu, naamini iko dhamira ya dhati kabisa ambayo tayari imeshaonekana hasa katika msimu uliopita wa 2018/2019, lakini zipo changamoto ambazo tungependa awamu hii wakati tunajiandaa tungeona mabadiliko makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mfumo uliotumika 2017/2018 wa kutoa pembejeo bure au karibu na bure au kuleta pembejeo ya ruzuku, ningependa kushauri watu wanaohusika ili waweze kuona namna sasa tunavyoweza kwenda kupata hizi pembejeo ili wakulima wetu waongeze uzalishaji katika zao hili la korosho ambalo kwa muda kidogo sasa ni kama hatufanyi vizuri sana kwenye uzalishaji. Kwa hiyo pendekezo langu kubwa ambalo ningependa kulitoa ni hilo kwa wale ambao wanahusika na zoezi hili la utoaji wa pembejeo na hasa ukizingatia katika hotuba hii suala la kilimo pia limegusiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia tunahitaji tuone maandalizi ya haraka sana, tuone namna ambavyo wadau wanaohusika na zao la korosho wanavyoweza kukutana na kuanza kufanya tathmini ya changamoto ambazo tumezipitia katika msimu. Ziko hoja za masoko, lakini pia ziko hoja zinazohusiana na namna bora ya kuendesha msimu kupitia Vyama vyetu vya Ushirika. Niwaombe watu wanaohusika waweze kupanga ratiba za haraka, lakini pia waweke katika kalenda za vikao tuweze kukutana mapema, tuweze kujadiliana yale yote ambayo mwaka huu yamejitokeza katika huu msimu, basi tuhakikishe msimu ujao wa 2019/2020, mambo haya machache ambayo yamejitokeza hayatojirudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala kubwa ambalo limezungumzwa kwa muda mrefu sana kuhusiana na korosho suala zima la kangomba, kangomba ime-trend sana, imezungumzwa sana, lakini yako maelezo ambayo sisi tunashukuru kupitia hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Waziri Mkuu na kupitia Bunge lako, tungependa sasa tushauri ili tuepukane na kangomba kwa kadri ya maelekezo yaliyotolewa. Yako mambo ya msingi ambayo yakifanyika tunaamini suala la kangomba msimu ujao, na maelekezo yaliyotolewa halitojirudia na kubwa ni hili la kupeleka pembejeo, kwa sababu sulfur zinavyokosekana hili limechochea wakulima wetu kuingia katika majaribu ya kuwapa wafanyabiashara korosho zao ili waweze kuhudumia mikorosho yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ili kuliepuka hili na kuwaepushia wakulima adha walioipata safari hii, basi ni vizuri sana tukaona namna ya kutengeneza hayo mazingira wezeshi ya kupanga vikao, ya kupanga bei, lakini pia ya kutoa pembejeo kwa wakati na kwa gharama nafuu ambazo zitaepusha wakulima kukutana na wafanyabiashara au watu ambao hawana nia nzuri ya kuwasaidia wakulima ambao kwa muda mrefu wamekuwa wanapata changamoto katika uzalishaji wa zao hili la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaishukuru sana Serikali kwa namna na nia njema waliyoonesha katika kuendelea kufungua na kuboresha Viwanda vya Kubangua zao la Korosho. Juzi Mheshimiwa Rais akiwa Newala kule Tandahimba amezindua na kuona Kiwanda kile cha Iyuri, lakini bado tuna maeneo mengine ambako kuna Viwanda ambavyo vilikufa na tayari Serikali imeshaonesha nia ya kuvirejesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nachingwea tunacho Kiwanda cha Mamlaka ya Korosho, bado Kiwanda kile kinacho uwezo mkubwa wa kuweza kuzalisha na tayari wapembuzi wameshafanya kazi ya kukikagua ili waweze kuona namna ya kukirejesha, lakini bado Mtama kuna Kiwanda na Lindi Mjini bado kiko Kiwanda ambavyo hivi vyote vikitengenezewa mazingira mazuri azma ya kubangua korosho ndani ya maeneo yetu itakuwa ni kubwa na hivyo tutaenda kuongeza thamani ya zao la korosho na pia tutaenda kuongeza ajira kwa vijana wetu na kuboresha mfumo mzima wa upatikanaji wa korosho katika mazingira yetu. Kwa hiyo, haya niliona niyazungumze kama sehemu ya mapendekezo ambayo ningependa Serikali iyachukue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nizungumzie ni suala zima la zao la mbaazi, bado wakulima wetu sisi ni wazalishaji wakubwa wa zao la mbaazi. Hapa tunapozungumza tuko kwenye msimu wa maandalizi, naomba kupitia Wizara ya Kilimo, ambayo iko chini ya Ofisi pia ya Waziri Mkuu na kwenye hotuba imezungumziwa, waone namna wanavyojipanga katika kuhakikisha hatuyumbi tena katika upatikanaji wa masoko hasa wa zao hili ambalo kwetu sisi ni muhimu sana na linazalishwa kwa wingi sana. Miaka mitatu iliyopita zao la mbaazi hatujafanya vizuri, kwa hiyo naamini wakati tunaelekea kwenye kuhitimisha hizi bajeti basi, tutapata maelekezo mazuri ya namna ambavyo tunajiandaa kwenda kununua zao la mbaazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba nizungumzie suala zima la miundombinu, Jimbo la Nachingwea, Jimbo la Liwale, Jimbo la Masasi kwa sehemu kubwa ndiyo wazalishaji lakini pia miundombinu yake sio rafiki sana. Naipongeza Serikali kwa sababu imeonesha nia ya dhati ya kujenga barabara ya lami kutoka Masasi kwenda Nachingwea, Nachingwea kwenda Ruangwa, Ruangwa kwenda Nanganga na tayari utaratibu wa kuitangaza hii barabara kwa ajili ya kupata mkandarasi ulishafanyika. Hata hivyo, mpaka sasa hivi ninavyozungumza bado sijaona taratibu zozote ambazo zinaendelea, kwa hiyo wakati tunaendelea kutaka kupitisha bajeti hii, niwaombe sana watu wanaohusika watoe maelekezo ya kina ya namna ambavyo wamejipanga kuanza ujenzi wa barabara hii ambayo ina kilomita karibu mia moja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Masala.

MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Spika, naomba nishukuru sana kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Maji. Naomba niungane na waliotangulia kuwapongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na msaidizi wake, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo amekuwa anaifanya katika kuhakikisha Watanzania wanapata huduma hii muhimu ya maji.

Mheshimiwa Spika, kipindi chote ambacho nimekuwa nasimama hapa nimekuwa ni mtu wa kuomba tu juu ya mahitaji ya jimbo ambalo ninaliongoza, lakini katika Wizara hii nitakuwa mtovu wa fadhila kama sitatoa neno la shukrani kwa Mheshimiwa Waziri, Mzee wangu Mheshimiwa Kamwelwe, kwa kweli, ametitendea haki watu wa Wilaya ya Nachingwea, mara zote ambazo tumemuomba mahitaji yetu amekuwa ni msikivu, lakini pia amekuwa ni mtu ambaye amejali sana kwa kufanya ziara si chini ya mara tatu katika Wilaya yangu ya Nachingwea kuja kuona hali ya upatikanaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika hili nilikuwa naomba kabisa nimpongeze na nimtakie kila la heri mzee wangu kwa kazi nzuri ambayo anaifanya na tunaendelea kumuombea mambo mazuri zaidi ya hapo alipo ili ikiwezekana basi mambo yakae sawa.

Mheshimiwa Spika, yako maeneo ambayo kimsingi tuliomba, moja ni eneo la utanuzi wa mtandao wa maji ya Mbwinji. Kwa mwaka jana alitutengea shilingi bilioni moja na katika fedha ile tulipata zaidi ya shilingi milioni 870 na hii imetuwezesha kutanua maji. Katika Wilaya yangu mimi viko vijiji takribani nane ambavyo toka uhuru wa nchi hii upatikane hawakuwahi kupata maji safi na salama, lakini sasahivi tunavyozungumza wananchi wa Kata za Naipanga, Rahaleo, Chiwindi, Nkotokuyana, Stesheni, Mtepeche, pamoja na maeneo yote yanayozunguka mradi huu sasa hivi wanapata maji safi na maji salama. Kwa hiyo, katika hili Mheshimiwa Waziri naomba upokee pongezi na salamu kutoka kwa wale wananchi ambao uliwatembelea mwaka jana na ukaenda kupanda kwenye yale matenki ya pale Chiumbati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nilitaka pia nione na nipongeze ni eneo la upatikanaji wa fedha abayo sasa hivi nafikiri wametutengea. Nimesoma katika kitabu hiki cha bajeti nimeona kuna shilingi bilioni mbili zimetengwa kwa ajili ya kuuendeleza mradi huu kwa ajili ya kuweka chujio ambalo litasaidia kupata maji mazuri zaidi. Kwa hiyo, sio fedha ndogo hii ni fedha kubwa na kwa uchapakazi ambao Mheshimiwa Mzee Kamwelwe ameendelea nao nina hakika fedha hii tutaipata kwa wakati, ili wananchi wa Masasi, Nachingwea, pamoja na Ruangwa ambao wananufaika na Mradi wa Mbwinji waweze kupata maji ambayo kimsingi ni mahitaji makubwa sana ambayo tumekuwa tunayahitaji.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo pia, nilitaka nilizungumzie, nimeangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nimeangalia kwenye kitabu ukurasa namba 120, nimeona fedha ambayo Wilaya ya Nachingwea tumetengewa, shilingi bilioni moja karibu na milioni mia mbili kwa ajili ya maji vijijini. Tunavyo Vijiji vya Mtua ambavyo kwa muda mrefu vimekuwa vinakosa maji, lakiini pia tunacho kijiji cha Ndomoni, tunacho Kijiji cha Marambo pamoja na maeneo mengine, yote hayo yatapata maji. Ila wito wangu Mheshimiwa Waziri, Mzee wangu Mheshimiwa Kamwelwe naomba nikuombe, mpaka sasa hivi wakandarasi ambao wamepewa kufanya kazi katika maeneo haya tayari tender zilishatangazwa.

Mheshimiwa Spika, tunaomba msukumo wako, ili kazi ya kupeleka maji kwa sababu fedha tayari mmeshatutengea, naomba kwa heshima na taadhima ifanyike, ili wananchi hawa waweze sasa kwenda kupata maji ambayo fedha yake kimsingi tayari hata mkurugenzi wangu mlishamuita na mmeshampa maelekezo juu ya kwenda kusimamia zoezi la kuanza kazi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, mradi huu au miradi hii ni muhimu sana na itawasaidia wananchi wa maeneo haya kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo nikuombe Mheshimiwa Waziri pale Nachingwea kuna eneo moja linaitwa Mnero Miembeni, kuna mradi mkubwa ambao mwaka jana ulikuwa unatengenezwa na mkandarasi mmoja ambaye kimsingi kazi yake mpaka sasa hivi bado haijakaa
sawa. Yapo maeneo ambayo amefunga solar ambazo haziwezi kusukuma maji na ule mradi ni mkubwa zaidi umetumia zaidi ya shilingi milioni 150, lakini mpaka sasahivi ninavyozungumza Mheshimiwa Waziri na ofisini kwako nilikuja, bado maji katika maeneo yale ya Mnero Miembeni ambayo yanahudumia vijiji karibu sita mpaka sasa hivi ninavyozungumza bado maji hayajaanza kutoka na yule mkandarasi ni kama tayari alishamaliza kazi.

Sasa tunaomba msukumo wako, tunaomba wataalam waje wachunguze ni sababu gani ambazo zimesababisha kufunga solar ambazo zinashindwa kufanya kazi tofauti na malengo ambayo yamkusudiwa.

Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali ni njema, nia ya wizara yako ni njema ndio maana ulitoa fedha. Mradi ule ulikuwa umeenda pia na maendeo ya Nditi kule ambako kimsingi Nditi maji yanapatikana, lakini katika eneo la Mnero Miembeni bado kumekuwa na changamoto ambayo nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri wakati unahitimisha hotuba yako basi utuahidi namna bora ambayo unaweza ukatusaidia, ili maeneo yale wananchi waweze kupata maji ambayo wewe mwenyewe umeyasimamia na mimi nashukuru sana umenipa ushirikiano katika kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka pia, niombe ni eneo la visima. Nilikuomba Mheshimiwa Kamwelwe visima na uliniahidi kwamba utatusadia tupate visima kwa baadhi ya vijiji ambavyo kwa muda mrefu tumekosa maji na uwezekano wa kupeleka maji haya Mbwinji utatuchukua muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, tunacho Kijiji cha Namanga, hali ni mbaya, wananchi wanatembea umbali wa kilometa karibu 40 kwenda kufuata maji. Hali ile kwa wale mama zetu kidogo imekuwa ni ya kukatisha tamaa. Nia yako ni njema na ulishaniahidi tangu mwaka jana kwamba utatusaidia. Nikuombe sana na ninaleta hili ombi tena, kwamba vile vijiji ambavyo uliniahidi kunipa visima angalao vinne, basi tutumie nafasi hii ili wale wananchi tuweze kuwasaidia na tuwatue mama zetu ndoo kichwani, ili waweze kufanya shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ambalo nilitaka nichangie ni eneo la mradi wa umwagiliaji. Ndani ya Wilaya ya Nachingwea tunayo miradi mikubwa miwili ya umwagiliaji, eneo mojawapo ni eneo la Matekwe. Mradi huu ni wa muda mrefu kwa kipindi cha nyuma tulishawahi kupata shilingi milioni 500, lakini mradi ulikoishia mpaka sasa hivi ni kama fedha imepotea. Pia pia Mheshimiwa Kamwelwe unakumbuka tulikupeleka eneo moja la Mitumbati pale ukatuahidi utatupa shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuukarabati na kuurejesha ule mradi katika hali yake ya kawaida, lakini mpaka sasa tunavyozungumza nimeangalia katika makabrasha yako sijaona kama umetukumbuka.

Mheshimiwa Spika, wale wananchi wamesimamisha shughuli zao za kilimo, lakini pia, tulikuwa tunatamani tuwarejeshe kwa sababu kipato chao kwa sehemu kubwa wanakipata kupitia maeneo yale. Mimi nikuombe sana mzee wangu na watu wa wizara muweze kuona namna ambavyo zile fedha ambazo tumeziomba zitakavyoweza kwenda kupatikana tuweze kurudisha ile miradi ya umwagiliaji ikae katika utaratibu ambao wananchi wetu wanaweza wakafanya shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, mimi naomba niunge mkono hoja na niwatakie kila la heri watu wa Wizara katika utekelezaji wa bajetio yao. Asante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi na mimi pia niweze kuchangia Wizara hii ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Wabunge wenzangu kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri na kubwa ambayo anaifanya ya kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora katika eneo hili la afya ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimpongeze kiupekee sana Waziri wa Afya, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu akisaidiana na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile kwa kazi nzuri na kubwa ambayo wanaendelea kuifanya ya kuhakikisha sekta ya afya inaendelea kutoa huduma kama ambavyo imeahidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mtovu wa fadhila kama sitasimama hapa na kutoa neno la pongezi kwa Serikali hii kutokana na kazi kubwa ambayo wameifanya. Wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwa sehemu kubwa wamekuwa wanapata huduma za afya katika hospitali kubwa ya Wilaya ambayo Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu mmetembelea mara kadhaa. Kwa kweli naomba nitoe neno la shukrani kutoka kwa wananchi wale kwa namna ambavyo mmejali kwa kuja kukagua mazingira, lakini pia kwa kusikiliza maombi mbalimbali ambayo tumeyatoa kwenu kama Wizara na kwa kweli mmetuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niliona nitumie nafasi hii kuwashukuru sana lakini bado tunaendelea kuwaomba yale ambayo tumeyaleta mezani kwenu basi muendelee kutuunga mkono ili wananchi wale waweze kupata huduma kama ambavyo tumeahidi. Hapa ninapozungumza sasa hivi, uko ujenzi wa Jengo la OPD kupitia shilingi milioni 400 ambazo zimetoka katika Serikali yetu. Lengo kubwa ni kuhakikisha huduma za afya kwa wananchi zinaendelea kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nishukuru wananchi wetu wamekuwa wanapata huduma pia katika Hospitali ya Rufaa pale Sokoine, Lindi. Hospitali ya Sokoine, Lindi sasa hivi ni kubwa na inatoa huduma katika maeneo mengi sana. Uboreshaji mkubwa umefanyika katika upatikanaji wa maji lakini pia uboreshaji wa mazingira yale ya hospitali ambayo wananchi wetu wengi wanaotoka katika Wilaya za Mkoa wamekuwa wanaenda pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi letu ambalo ningependa kuliwasilisha kwenu ni kutuongezea wataalam hasa madaktari bingwa katika hospitali. Madaktari hawa watakwenda kuhakikisha wananchi wanaotoka katika maeneo ya Nachingwea, Liwale na maeneo mengine hawaendi sasa Muhimbili badala yake huduma zote wanazipata katika hospitali ile ya Rufaa ya Sokoine ambayo Serikali imefanya kazi kubwa sana kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka nijaribu pia kutoa ushauri na kuomba watu wa Wizara, Mheshimiwa Ummy utakumbuka tulifanya ziara Naipanga. Naipanga ni sehemu ya Tarafa lakini idadi ya wananchi pale ni zaidi ya watu 14,000, umuhimu wa kujenga kituo cha afya na kwa ahadi ya Serikali nafikiri pia utakumbuka na Naibu wako Waziri Mheshimiwa Dkt. Ndugulile tulifanya ziara pale. Nawaomba sana hebu tufanye yale ambayo tuliwaahidi wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama wananchi wa eneo lile tayari tumeshaanza kufanya jitihada za kuhakikisha tunatenga eneo. Hata hivyo, kwa sababu lengo ni kupandisha hadhi ile zahanati iliyoko basi, naamini ahadi ile wakati mnaenda kuhitimisha basi hamtatusahau ili wananchi waweze kupata huduma pale wasitembee umbali mrefu wa kwenda Hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenda Hospitali ya Wilaya maana yake tunaweka wingi wa watu usiokuwa na ulazima. Kwa hiyo, ili kuepuka umbali lakini pia kuwasogezea wale wananchi huduma, naomba niwakumbushe kwa sababu ni eneo ambalo tayari wenyewe mmeshaona mazingira halisi ya pale na namna ambavyo wananchi wamekuwa wanapata shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kiko kituo kingine cha Marambo. Kituo hiki kiko ndani ya Tarafa pia ya Ruponda, idadi kubwa ya wananchi wanatembea umbali mrefu kwenda Hospitali ya Wilaya. Naomba kupitia bajeti hii na mikakati mingine ambayo mnaendelea nayo kama Wizara, basi muone umuhimu pia wa kutuunga mkono ili tuweze kupandisha na kuboresha kituo kile cha afya kiweze kutoa huduma kwa wananchi wote wanaotoka Ukanda wa Marambo. Kule watahudumia wananchi wanaotoka Mkoka, Marambo yenyewe, Chilola pamoja na maeneo ya jirani ambayo wananchi wamekuwa wanategemea kituo kile kwa ajili ya kupata huduma zote muhimu ikiwemo upasuaji pamoja na kupata tiba nyingine muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo niliona pia nilizungumze, ndani ya Wilaya ya Nachingwea tuna kituo cha Mission cha Mnero. Kituo hiki ni cha zamani kidogo na kinahudumia wananchi wanaotoka Tarafa ya Ruponda. Kwa muda mrefu kituo hiki huduma zake zimekuwa za kusuasua. Tunashukuru Serikali kwa sababu imekuwa inapekeleka Busket Fund ingawaje siyo fedha ya kutosha sana lakini jitihada zozote zitakazofanyika za kuhakikisha kituo kile kinapatiwa fedha za kutosha naamini kitaenda kuondoa uwingi wa watu wanahitaji huduma katika Hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, pamoja na watalam wako hebu nawaomba sana pamoja na mikakati mingine mnayoendele a kuifanya, hebu tukiangalie kituo hiki ambacho kwakweli kinatusaidia sana sambamba na kituo kile cha Ndanda ambacho nacho pia kinafanywa kwa mtindo huo kwa sababu kiko chini ya Mission lakini bado mkitoa fedha za kuhakikisha huduma zinapatikana katika maeneo haya basi wananchi wetu wengi wataenda kunufaika na huduma bora ambazo zitaenda kutusaidia kuondokana na kero za wananchi kukosa huduma bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nikuombe Mheshimiwa Waziri, bado tunachangamoto ya huduma ya magari kwa ajili ya kusafirishia wagonjwa. Kwanza katiak hospitali ya wilaya bado ambulance tuliyonayo ni moja, haitoshelezi mahitaji hivyo tunalazimika kuchukua magari mengine nje ya ambulance kwa ajili ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunacho kituo cha afya cha Kilimarondo ambacho ninaishukuru Serikali imetupatia milioni 400 kituo kimekamilika lakini bado tuna changamoto ya kupata gari ya wagonjwa na ni umbali wa zaidi ya kilometa 120 ambayo wananchi wale kwa kukosa gari wamekuwa wanapata changamoto kubwa kwa muda mrefu. Kwa hiyo, ninaomba pamoja na kazi nzuri iliyofanyika, bado nilete maombi kwenu watu wa Wizara muweze kutusaidia katika mgao wa magari basi maeneo haya mawili yapate magari ya wagonjwa ili wananchi waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza wa hotuba ya Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Ya kwangu nilikuwa naomba nichangie katika maeneo makubwa manne.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ambalo nilitaka nichangie ni eneo linalohusu Mamlaka ya Biashara - TANTRADE. Hawa ukisoma kwa mujibu wa kazi zao ambazo wanazifanya, kazi kubwa mbili za msingi kazi ya kwanza ni kufanya utafiti wa masoko, lakini pia mamlaka hii imepewa kufanya kazi ya intelijensia ya kujua kwa wakati tuliokuwa nao dunia inataka nini katika eneo la bidhaa. Sambamba na hili bado mamlaka hii imekuwa inafanya kazi kwa ajili ya kutangaza bidhaa zetu kupitia maonesho ambayo yamekuwa yanafanyika pale Sabasaba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hizi zote zinaenda vizuri, lakini bado naomba nijielekeze zaidi katika hizi kazi kubwa mbili. Kwa muda mrefu tumekuwa na wakulima lakini sehemu kubwa Watanzania tumekuwa tunajishughulisha na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ikiwezo hizi bidhaa za mazao. Sasa yako maeneo ambayo kidogo nashangaa kuona namna ambavyo mamlaka hii inavyofanya kazi na namna ambavyo wakati mwingine ilivyoshndwa kusaidia nchi yetu katika kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mifano katika maeneo makubwa mawili, mimi nina wakulima ambao wanalima zao la mbaazi. Zao hili kwa muda mrefu limelegelega kupata bei na kwa miaka ya karibuni mitatu iliyopita tumeshindwa kabisa kuuza mbaazi zetu, sasa kama mamlaka hii ingekuwa inafanya kazi yake ipasavyo na kama ingekuwa imetekeleza wajibu wake wa kufanya utafiti au uchunguzi juu ya masoko ya zao hili na namna ya kuishauri Serikali nafikiri wakulima wetu leo hii wasingekuwa wanapata changamoto ya wapi wataenda kuuza bidhaa zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wakulima wetu wako njia panda wanashindwa kujua kama waendelee kuzalisha mbaazi au wabaki kama ambavyo walikuwa wanafanya zamani kutumia mbaazi kama mboga. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa hebu atueleze mamlaka hii inatekelezwa ipasavyo na kama inatekelezwa kwa nini kwa miaka minne mfululizo tumeshindwa kupata jibu la uhakika juu ya hatma ya zao hili ambalo kwa baadhi ya wakulima wetu wamekuwa wanashiriki kulifanya na hatimaye tumeingia hasara ambayo kimsingi bado tumeshindwa kuwasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, mwaka jana kwa maana ya msimu wa korosho nafikiri wewe mwenyewe utakuwa ni shahidi, Mawaziri wetu wamekuwa wanagongana juu ya bei ya korosho. Kama mamlaka hii ingefanya intelijensia yake ya kuchunguza bei katika soko la dunia, lakini pia kuchunguza uhitaji katika mahitaji ya kidunia, naamini kusingekuwa na mgongano wa bei ambao umesababisha leo hii wakulima wetu wengi washindwe kupata bei ambayo ilikuwa inatazamiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kwa heshima na taadhima basi Mheshimiwa Waziri wa Biashara kaka yangu Mheshimiwa Kakunda aweze kutueleza, hawa watu wa TANTRADE ukiondoa kufanya maonesho ya biashara ambayo sasa hivi kwa sehemu kubwa ni kama wanachukua tu wachuuzi hata wauzaji wa mitumba wako pale uwanja wa Sabasaba wanafanya shuguli zao na mambo mengi ambayo yanakwenda pale kufanyika ya kutangaza dawa na vitu vyepesi vyepesi tu, ambavyo kimsingi mimi nilikuwa naona jukumu hili la msingi kama wangezingatia, kama wangewezeshwa basi naamini leo hii sisi tungekuwa tunajua tuzalishe tani ngapi za mbaazi na zitakwenda wapi kwa sababu tayari watakuwa wameshatupa bei na uelekeo wa mazao haya tutayapeleka wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwombe sana kaka yangu Mheshimiwa Kakunda atakapokuja kuhitimimisha basi atueleze na kama hawajajipanga katika uelekeo huo, basi hebu tuwasaidie na akiwasaidia hawa kuwaweka vizuri maana yake watawasaidia hata watu wa Wizara ya Kilimo ku-forecast bei, lakini pia kupanga mipango mizuri ambayo haitaenda kuwaumiza wakulima wetu kama ambavyo sasa hivi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo naomba nichangie, ni eneo lingine linalohusu watu wa SIDO. Nilikuwa najaribu kupitia hapa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kuna huu Mfuko wa Maendeleo ambao unakopesha wakulima wa NEDF. Naomba nimpongeze sana na nilikuwa nafuatilia hapa takwimu za mikopo midogo midogo ambayo imekwenda kwa wajasiriamali. Hata hivyo, concern yangu kubwa ambayo nataka tuweze kushauriana vizuri ni tuone namna gani mfuko huu wa SIDO unavyochangia na unavyosambaa kuwafikia wale wanyonge walioko maeneo ya mbali kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa napitia takwimu nyuma za hiki kitabu nione katika Mkoa wa Lindi mathalani, Wilaya ya Nachingwea, ni wajasiriamali wangapi wadogo wadogo ambao wamenufaika na Mfuko huu wa SIDO, lakini ni kiasi gani cha fedha ambacho ndani ya miaka hii miwili, mitatu kimeenda kwa wakulima. Niwapongeze kwa sababu fedha nyingi zimekwenda, lakini uwiano wa namna ambavyo tumewafikia wajasiriamali wadogo wadogo kidogo unanitia mashaka. Sasa naomba kipaumbele chetu kijielekeze kwa kadri ya uzalishaji tunaoufanya na namna ya kuwezesha wajasiriamali wadogo kwa shughuli za uzalishaji wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mamalishe lakini pia tunao watu wadogo ambao wanafanya kazi ya ubanguaji wa korosho kule kwetu. Haya makundi yote kama tungeweka utaratibu mzuri wa kugawa hizi fedha naamini tungeweza kuwafikia wanyonge wengi sana walioko kule chini badala ya kukopesha tu katika maeneo makubwa au maeneo ya mijini ambako hawa ndiyo wamekuwa wanajua fursa na wamejua kuzichangamkia na kuacha wakulima wetu wadogo wadogo amabo wako katika maeneo yale ya mikoani na wilayani kule chini. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri naomba sana watakapokuja kuhitimisha watuwekee utaratibu mzuri ambao utapelekea hata wale wakulima na wajasiriamali wadogo wadogo walioko chini wapate kunufaika na Mfuko huu wa Maendeleo kwa ajili ya kukopesheka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ambalo nataka nichangie ni eneo la mradi wa matrekta ya URSUS. Naomba nipongeze mradi huu wa matrekta ya URSUS ambao uko pale Kibaha. Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara yake tunatambua jitihada kubwa ambazo wamekuwa wanazifanya, lakini bado naomba tuone namna ambavyo mradi huu unavyoweza kuwafikia pia walengwa ambao ni wakulima walioko katika maeneo ya pembezoni. Kibaha ni center, mkulima anayetoka Mtwara, Ruvuma, Lindi ni nadra sana kufahamu fursa inayoweza kupatikana kupitia mradi huu wa matrekta. Matrekta haya ni bora na tulitamani sana yangewafikia wakulima wetu ili waweze kuzalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ukienda kwenye baadhi ya maeneo trekta ni ya kugombaniana. Wakulima hawana access ya kupata vyombo hivi kwa ajili ya kulima kilimo cha kisasa. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri ikimpendeza hebu tuone utaratibu wa kufungua center katika baadhi ya maeneo. Kwa mfano tunaweza tukaweka center ya Kusini ambayo itajumuisha mikoa mitatu ya Lindi, Mtwara, Ruvuma kule at least wakaweka sample ya matrekta na utaratibu wa namna ambavyo wakulima wetu wanavyoweza kukopa au kuweza kuyapata haya matrekta kwa gharama nafuu zaidi, tofauti na ilivyo sasa hivi mtu wa kutoka kule mbali aweze kuyafuata haya matrekta Kibaha au maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi mradi mkubwa ambao tunategemea kukopa matrekta ni wa SUMA JKT ambao bado haufanyi vizuri sana. Hata hivyo, kupitia mradi huu naamini Serikali kama mtaweka mazingira mazuri, basi wakulima wetu wengi watapata access ya kufikia na kuweza kuchukua matrekta ambayo yatawasaidia katika uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ambalo nilitaka….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, kengele ilishagonga.

MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)