Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Juliana Daniel Shonza (43 total)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, nina nyongeza ndogo. Kwanza kabisa kwa kifupi sana na mimi nimpongeze sana dada yangu Juliana na nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuona vijana wanaweza kumsaidia. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa je, Serikali ipo tayari kuweza kuitumia Miji aidha Mji wa Dodoma au Singida kwa sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Spika, inajulikana kabisa kwamba Singida sasa hivi tayari tuna kiwanja cha kisasa kabisa cha Namfua ambacho kimeshafanyiwa miundombinu ya kisasa na Singida tunaendelea tuna hoteli za kisasa ambazo zimejengwa na wazalendo.
Mheshimiwa Spika, Dodoma pia tunaona Serikali yetu imehamia hapa na Mheshimiwa Rais anakuja hapa, Waziri Mkuu tayari tunae hapa na Makamu wa Rais anakuja. Sasa kwa nini Serikali isiamue tu kwa makusudi kuchagua mikoa hii miwili kati ya Singida au Dodoma kufanyika mashindano ya AFCON 2019? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kuweza kuwapongeza Wabunge wote wa Mkoa wa Singida kwa jitihada zao nzuri ambazo wamezifanya katika kurekebisha Uwanja wa Namfua. Nichukue nafasi hii kuomba Wabunge wote lakini vilevile mikoa yote ya Tanzania kuweza kuiga mfano huu mzuri ambao umeoneshwa na Wabunge wa Singida lakini vilevile wananchi wa Mkoa wa Singida. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nikienda sasa kwenye swali lake la msingi ambapo amependekeza kwamba nini Uwanja wa Namfua, Singida usitumike katika mashindano haya. Niseme kwamba moja ya vigezo ambavyo huwa vinazingatiwa katika kuchagua haya maeneo. Jambo la kwanza ni kuhakikisha kwamba huo mji ambao unapendekezwa uweze kuwa na viwanja ambavyo vinakidhi ubora wa Kimataifa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kigezo cha pili ni lazima kwamba mji huo uweze kuwa na hoteli ambazo zitaweza ku- accommodate wageni wote ambao watakuja katika mashindano hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme kwamba kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi, Mheshimiwa Kingu kwamba sasa hivi kuna Kamati ambayo imeundwa na Mwenyekiti wa hiyo Kamati ni Waziri wangu Dkt. Mwakyembe.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme kwamba nimtoe hofu mimi kama Naibu Waziri nitamshauri Waziri wangu Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe sasa aangalie namna gani kwamba ile Kamati ambayo imeundwa ifike Singida ili kuweza kukagua ile miundombinu ya michezo ambayo ipo katika Mkoa wa Singida. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika swali la pili ametaka kujua kwamba kwa nini Dodoma isitumike katika mashindano haya. Kwanza napenda nichukue nafasi hii kuweza kumpongeza sana kwa dhati Mheshimiwa Rais kwa sababu kwa jitihada zake yeye binafsi sasa hivi Dodoma tunajengewa uwanja mkubwa kabisa wa Kimataifa wa michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niseme kwamba hii inaonesha kabisa kwamba Rais wetu ni Rais ambaye ana ushawishi mkubwa sana kwa Mataifa ya nje lakini inadhihirisha kwamba Rais wetu ni mwanadiplomasia na ni Rais ambaye anapenda michezo ndio maana ameweza kumshawishi Mfalme wa Morocco kuja kutujengea kiwanja hapa katika Mkoa wa Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niseme kwamba wazo lake ni zuri na niseme sisi kama Wizara tunachukua hilo wazo lakini kama ambavyo nimesema awali, kwamba uwanja huo unajengwa kwa msaada wa Mfalme wa Morroco. Kwa hiyo, sisi kama nchi hatuwezi kumpa deadline kwamba uwanja huo ukamilike ndani ya muda gani.
Mheshimiwa Spika, tunachokifanya na nimwombe kabisa Mheshimiwa Kingu kwamba endapo uwanja huo utakamilika kabla ya hayo mashindano kufanyika mwaka 2019, basi tutaangalia ni namna gani ambavyo uwanja huo unaweza kutumika katika mashindano hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali ambayo yanatia matumaini, nina maswali madogo ya nyongeza.
Swali la kwanza, wakati redio ya TBC wanatumia mawimbi ya short wave na medium wave mawasiliano yalikuwa mazuri. Je, hawaoni kwamba kuhamia kwenda digital inaweza ikawa ni changamoto hata kwa maeneo mengine yaliyoko pembezoni katika Taifa letu? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 18(b) tunayo haki ya kupokea na kupata taarifa, sasa anawaambia nini wakazi wa Mlalo ambao wako pembezoni mwa nchi jirani ya Kenya ambao hawapati habari za Taifa lao na je, hawaoni kwamba hii inahatarisha usalama wa Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii ya kuweza kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rashid Shangazi kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia kwa umakini kabisa matatizo ya wananchi wa Jimbo la Mlalo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba baada ya kupokea majibu mazuri kabisa ya Serikali nilitegemea kwamba Mheshimiwa Shangazi atakuwa hana maswali ya nyongeza. Kwa sababu ameuliza maswali mawili, naomba nimjibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kweli kwamba kuhama kutoka kwenye mfumo wa analogy kwenda kwenye digital imepelekea kuweza kupunguza usikivu wa redio hii ya TBC. Changamoto kubwa ambayo ilikuwepo ni kwamba mitambo mingi ambayo ilikuwa inatumika ilikuwa ni mitambo ambayo imechoka, mibovu ukizingatia kwamba mitambo hiyo ilikuwa ni ya muda mrefu sana.
Kwa hiyo, hata linapokuja suala zima la kutafuta vipuri kwa ajili ya kufanya marekebosho ya mitambo hiyo, ilikuwa ni ngumu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Rashid Shangazi kwamba tatizo hilo kwa sasa hivi TBC imelichukua kwa kina na inalifanyia kazi na mpaka sasa hivi katika mikoa ya Arusha, Dodoma, Mwanza pamoja na Kigoma tumeanza utaratibu wa kuboresha mitambo hiyo ili kuhakikisha kwamba matangazo haya ya TBC Taifa pamoja na TBC FM yanawafikia wananchi kama ambavyo inatakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la pili, ametaka kujua umuhimu wa chombo hiki cha Taifa, TBC kwa maeneo ambayo ni ya mipakani. Mheshimiwa Shangazi, Serikali hii ya Awamu ya Tano inatambua kabisa kwamba wananchi wote ambao wanakaa maeneo ya mipakani wana haki ya kupata taarifa kama ambavyo wananchi wengine wanakaa katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia hilo, kuna mkakati wa TBC ambao umeshaanza kufanyika katika maeneo ya mpakani, nikianza na eneo la Rombo, lakini ukienda na eneo la Namanga, Tarime pamoja na Kakonko, tayari ufungaji wa mitambo mipya ya TBC umeanza kufanyiwa kazi. Tunaamini kwamba mitambo hii itakapokamilika, kwa kiasi kikubwa sana itasaidia kumaliza tatizo hili za usikivu kwa chombo hiki cha TBC.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Shangazi aliuliza kwa upande wa Lushoto. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba tayari shilingi milioni 50 imeshatengwa kwa ajili ya kumaliza tatizo la usikivu katika Wilaya hiyo ya Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kabisa Mheshimiwa Shangazi kwamba eneo hili la Kwamashai ambalo limechaguliwa kuhakikisha kwamba mtambo huu unawekwa, ni eneo ambalo limefanyiwa utafiti wa kina na imeonekana kabisa kwamba mtambo huo ukijengwa hapo, basi maeneo yale ya Lukozi, Mnazi pamoja na Lunguzi ambako imepakana kwa ukaribu kabisa na kijiji ambacho kiko kwenye nchi ya Kenya watapata matangazo ya TBC kama inavyotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina mswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, katika uwanja huo mimi kama Mbunge nilitoa hela yangu mwenyewe shilingi milioni kumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukimuona mtu anatoa hela yake mfukoni kupeleka kwenye project ya wananchi kwa zama hizi ujue kilio hicho ni kikubwa sana. Chunya ni Wilaya ambayo ni kongwe sana, sasa hivi ina miaka 76. Viongozi wengi wa nchi hii akiwemo Profesa Mark Mwandosya amesoma Chunya na viongozi wa kidunia akiwemo aliyekuwa Rais wa makaburu wa mwisho Pieter Botha alizaliwa Chunya na kusoma Chunya. Kwa hiyo, Chunya ni Wilaya ambayo inatakiwa iangaliwe kwa huruma sana. Serikali inasemaje kuhusu kututafutia Chunya wafanyabiashara wakubwa wanaoweza kutusaidia kujenga uwanja huo ili waweze kutangaza biashara zao? La kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri anasemaje kuhusu kuja Chunya aje auone uwanja huo ili awe na uelewa mkubwa na mpana kuhusu uwanja huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa mzee wangu Mheshimiwa Mwambalaswa kwa jitihada zake kubwa ambazo amekuwa akizifanya katika kuboresha miundombinu ya michezo katika jimbo lake. Niseme wazi kabisa kwamba Wizara yangu pia inayo taarifa kwamba Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na wananchi wa Wilaya ya Chunya na Jimbo la Lupa wamechangia kiasi cha shilingi milioni 224, ambazo kati ya hizo milioni kumi ametoa Mbunge wa Jimbo la Lupa Mheshimiwa Mwambalaswa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pia nichukue nafasi hii kuweza kuomba Wabunge wote kuiga mfano huu mzuri ambao Mheshimiwa Mbunge ameuonesha, lakini vilevile kuiga Halmashauri zote nchini zichukue mfano huu mzuri ambao umeonyeshwa na Halmashauri ya Wilaya ya Chunya katika kuwashirikisha wadau katika kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu ya michezo.
Kuhusu swali lake la kwanza ambalo ameuliza kuomba wadau, kwamba Wizara imsaidie kuweza kutafuta wadau. Mimi niseme kwamba Mheshimiwa Mbunge Wizara yangu iko tayari kabisa kushirikiana pamoja na wewe, lakini vilevile na Halmashauri ya Wilaya ya Chunya na Jimbo la Lupa kuhakikisha kwamba tunahamasisha wadau mbalimbali waweze kujitokeza katika kuchangia ujenzi huo wa uwanja wa michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ombi lake la pili, niseme kwamba Mheshimiwa Mbunge mimi nikutoe wasiwasi, na ni mwezi wa 12 tu nilikuwa katika Wilaya ya Mbeya Vijijini. Kwa hiyo, niseme kwamba tutakapotoka hapa naomba tukutane tukae, tujadili, tuongelee ratiba kwamba ni lini ili na mimi niweze kuja kujione uwanja huo wa Lupa.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa vijana wetu wanaanza vipaji wakiwa mashuleni, je, Serikali ina mpango gani kuipa sekta ya michezo hasa mashuleni ili angalau vijana hao tuwakuze katika vipaji vya michezo ili tuweze kufikia kama nchi ya Brazil?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri ambalo ameuliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Wizara kupitia Serikali tuna mpango mzuri sana wa kuhakikisha kwamba vijana wetu waliopo shuleni wanashiriki katika michezo. Sasa hivi ninavyoongea tayari Wizara kwa kushirikiana na Serikali tumesharejesha ile michezo ya UMISETA na UMITASHUMTA katika mashule yetu. Haya ni mashindano ambayo kwa kiasi kikubwa sana yanasaidia kuibua vipaji vya vijana. Tumeshuhudia kwamba michezo hiyo inakwenda vizuri na wanafunzi wengi wamekuwa wakishiriki na vipaji vingi vya vijana vimeendelea kujitokeza. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikutoe hofu kwamba Wizara tuna mikakati mizuri na tutaendelea kushirikiana kuhakikisha kwamba tunaedelea kuinua vipaji vya vijana wetu ambao wapo mashuleni, ahsante sana.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na niipongeze Serikali kuwa wazi kwenye swali hili. Pia ni-declare interest, mimi ni Mwenyekiti wa Chama cha Soka, Mkoa wa Singida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Baraza la Michezo la Taifa Na. 12 ya mwaka 1967 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 1971 na Kanuni za Usajili wa Vyama vya Michezo, Namba 442 ya mwaka 1999, kifungu cha 7(2)(c)(ii), inatambua mamlaka ya Waziri na Waziri ndiyo mwenye maamuzi ya mwisho ya vyama vya michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini viko baadhi ya vyama katiba zao hazitambui mamlaka ya Waziri na vyenyewe ndiyo vyenye mamlaka ya mwisho ikiwemo TFF. Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana, ikikupendeza kama utakuwa tayari kulinda, kuheshimu na kusimamia sheria hii iliyotungwa na Bunge na kuhakikisha vyama hivi kwenye katiba zao zinatambua role ama wajibu wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, Serikali imekiri wazi katika ruzuku ambayo inatolewa TFF ni zaidi ya bilioni 10 na ile dola milioni tatu tunazungumzia karibu bilioni saba, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, kama utakuwa tayari uiombe TFF ilete mpango kazi kwenye mikoa yetu ili tuweze kujua fedha hizi zinatumikaje. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Sima kwa sababu amekuwa ni mwanamichezo mahiri na vilevile ni mdau mkubwa sana wa michezo katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na kujibu swali lake la kwanza ambalo ametaka kujua kama kuna vyama vya mpira ambavyo havitambui mamlaka ya Waziri. Mimi niseme kwamba tunatambua kabisa kwamba TFF pamoja na viongozi wake wote wanapaswa, wanalazimika na hivyo wanatambua mamlaka ya Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani? Ukisoma Katiba ya TFF, Ibara ya 1(2) inasema kwamba TFF ni chombo cha mpira ambacho kimesajiliwa chini ya Sheria ya Baraza la Michezo ya mwaka 1967 kama ambavyo umesema na marekebisho yake ya mwaka 1971. Kwa maana hiyo sasa, kimsingi kwa sababu Baraza la Michezo ambalo ndiyo ambalo linasajili TFF liko chini ya Wizara ya Habari, kwa maana lipo chini ya Waziri husika mwenye dhamana ya michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwa sababu TFF iko chini ya Baraza la Michezo, kwa hiyo, kimsingi ni kwamba TFF inapaswa kutambua mamlaka ambayo Waziri kwa maana ya Serikali inayo. Naamini kabisa kwamba TFF inatambua mamlaka ya Waziri kwa sababu ni takwa la kikanuni na kikatiba na wanapaswa kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija kwenye swali lako la pili ambapo unataka kujua hizi fedha za FIFA Forward ambazo zimetolewa, unaiomba Serikali iweze kuishauri TFF iweze kutoa mchanganuo wa fedha hizo mapema. Mheshimiwa Sima natambua kabisa kwamba wewe ni Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu katika Mkoa wa Singida na kwa jinsi mimi ninavyotambua ni kwamba humu ndani tuna Wabunge wengi ambao ni viongozi wa vyama vya mipira. Kwa hiyo, najua kabisa kwamba ninyi kama Wenyeviti pamoja na Makatibu ndiyo mhimili mkubwa kabisa wa TFF lakini kimsingi ninyi ndio washauri wakubwa wa TFF. Kwa hiyo, kwa sababu TFF ina taratibu zake, ina mikutano yake ambayo huwa mnakaa na kila mwaka huwa mnakutana, mna mkutano wa robo mwaka, nusu mwaka pamoja na wa mwaka, naamini mtakapokutana ninyi mna nafasi kubwa kabisa ya kuweza kuishauri TFF ili kuweza kuandaa huo mchanganuo wa fedha.
Niseme kabisa sisi kama Serikali tumelipokea wazo lako na tunakubaliana kabisa na wazo lako kwa sababu tunajua kwa namna moja au nyingine litasaidia kuweka uwazi wa mapato na matumizi na kuondoa sintofahamu ambazo zilikuwepo siku za nyuma. Ahsante. (Makofi)
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza kwa kuwa luninga zinapoteza watoto wetu katika kupotosha watoto wetu katika maadili, je, Serikali ina mkakati gani wa kutusaidia katika suala hili?
Swali la pili, kuna changamoto katika wasanii wa muziki hasa katika nyimbo zao zina matusi, je, Serikali itatusaidiaje kwa sababu wanawake wanavaaa mavazi ambayo hayana staha Serikali itatusaidiaje kusudi waweze kuacha mambo hayo?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi kuweza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri sana, tumefaidika sana kama Wizara tunapopata maswali kama haya ningeweza pia kuweza kumshauri Mheshimiwa Waziri kama kuna uwezekano Mheshimiwa Nuru Awadhi aweze kuwa Balozi wa Maadili katika Bunge hili.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameelezea kwamba luninga zinasaidia sana katika kupotosha mmomonyoko wa maadili katika Taifa letu na mimi niseme kwa namna moja ama nyingine nakubaliana na mawazo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyasema, lakini hilo huwa linatokea tu pale ambapo kunakuwa hakuna chombo maalum cha kuweza kusimamia maudhui mbalimbali ambayo yanarusha na vyombo vyetu vya luninga. Kwa kutambua hilo na ndiyo maana Serikali imeunda vyombo viwili ambavyo ni TCRA pamoja na Bodi ya Filamu ambavyo vyote hivi vina lengo kubwa la kuhakikisha kwamba vinasimamia maudhui yanayorushwa katika vyombo vyetu vya habari. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niseme kwamba pamoja na changamoto hizo, Wizara tumeendelea kuhamasisha jamii kwa ujumla kuhakikisha kwamba suala la maadili ni suala ambalo lazima jamiii kwa ujumla wetu kuendelea kulifanyia kazi siyo suala tu la Serikali kama ambavyo nimejibu kwenye jibu la msingi kwamba ni suala ambalo la Serikali, lakini vilevile pamoja na jamii nzima kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika, habari njema ni kwamba Wizara kwa sasa hivi imeandaa kanuni mbili ambazo tunaamini kabisa kwamba kanuni hizo ambazo ni kanuni zinazosimamia maudhui katika redio, maudhui katika mitandao ya kijamii na tunaamini kabisa kwamba kwa kupitia kanuni hizi itakuwa ni muarobaini wa kuhakikisha kwamba mmomonyoko wa maadili katika Taifa letu unadhibitiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nipende kuchukua nafasi kuweza kuomba vyombo vyote vya habari viweze kuzingatia kanuni hizo ili kuhakikisha kwamba tunatunza maadili ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili ametaka pia kuweza kujua kwamba kumekuwa na tatizo la nyimbo ambazo haziendani na maadili ya Taifa letu hususani wanawake ambao wanavaa mavazi ambayo siyo ya staha.
Mheshimiwa Spika, mimi niseme kwamba sisi kama Serikali tunatambua kwamba tuna changamoto hiyo na kitu ambacho tumekifanya kwa sababu tuna vyombo vyetu viwili ambavyo ni vyombo vinasimamia maudhui kwa wasanii kwa maana ya BASATA pamoja na Bodi ya Filamu. Hivi vyombo viwili vimekuwa vikisisitiza mara kwa mara kuhakikisha kwamba wasanii kabla hawajatoa nyimbo zao wanapeleka nyimbo zao BASATA, wanapeleka video zao Bodi ya Filamu ili ziweze kuhaririwa na ziweze kupewa madaraja.

Mheshimiwa Spika, jambo la kusikitisha ni kwamba...
Mimi nikushukuru lakini niseme kwamba tumekuwa tuna changamoto kubwa sana k wasanii wetu hawapeleki nyimbo zao kwenda kuhaliliwa BASATA naomba kuchukue nafasi hii kuweza kuwaambia kwamba wasanii wote wahakikishe kwamba wanapeleka nyimbo zao BASATA ili ziweze kuhaririwa kabla hawajaanza kuchukuliwa hatua. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote naomba nitoe pole sana kwa familia za wasanii wenzangu, Jebby Mubarak na Agnes Gerald Masogange ambao wametangulia mbele za haki. Mungu awalaze mahali pema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba moja, pamoja na jitihada hizo tunazoziona za watu mmoja mmoja, wanariadha kuweza kufanya vizuri katika michezo mbalimbali, lakini imekuwa tabia ya Watanzania kupeleka timu mbaimbali kwenye mashindano mengine bila kuwaandaa.
Je, kwa nini sasa Serikali isiache kuwapeleka kwanza wanamichezo hao huko nje mpaka ihakikishe imewaandaa na kuweza kufanikiwa kuleta medali na kuitangaza vizuri Tanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba mbili, changamoto kubwa ya wanamichezo wa Tanzania ni viwanja kukosa ubora na nadhani ile shilingi trilioni 1.5 ingeweza kupunguza kwa kiasi kikubwa sana changamoto hiyo. Mara baada ya mfumo wa chama kimoja kusitishwa mwaka 1992 Chama cha Mapinduzi kimeonekana kuhodhi viwanja vikubwa karibu vyote vikubwa hapa nchini na kushindwa kuviendeleza…

MHE. JOSEPH L. HAULE: Je, hamuoni kwamba huu ni wakati muafaka sasa wa Chama cha Mapinduzi kurudisha viwanja vya michezo hivyo Serikalini ili viweze kutumika na Watanzania wote kwa ujumla? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa maswali mazuri ambayo yameulizwa na kaka yangu Profesa Jay. Nikianza na swali lake la kwanza ambapo ametoa ushauri kwamba kwa nini Serikali haipeleki wanamichezo nje kwa ajili ya kwenda kufanya maandalizi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba ushauri ambao ameutoa ni mzuri lakini nachukua pia nafasi hii kuweza kumtoa hofu kwamba katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 kwa sababu sisi kama nchi tunajua kabisa vijana wetu wa Serengeti Boys wanakabiliwa na mashindano makubwa na AFCON ambayo Tanzania itakuwa ni mwenyeji mwaka 2019. Kwa hiyo sisi kama Serikali kwa kushirikiana na TFF tuko kwenye mpango wa kuwachukua vijana wetu kuwapeleka Sweden kwa ajili ya kwenda kupata hayo mazoezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili ambapo amedai kwamba viwanja vingi vinamilikiwa na Chama cha Mapinduzi, niseme kwamba imekuwa ni Sera ya Michezo ya mwaka 1995 kuhamasisha wadau wote kuwa vyama vyote na taasisi zote vina hali ya kuweza kumiliki viwanja vya michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, viwanja vyote ambavyo vinamilikiwa na Chama cha Mapinduzi vinamilikiwa kwa halali na ni haki yao na hakuna hata kiwanja kimoja ambacho kimeporwa na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nachukua nafasi hii kuweza kuhamasisha Wabunge wote ambao mpo ndani ya Bunge hili, Halmashauri zote, wadau na taasisi zote kuhakikisha kwamba vinatenga maeneo kwa ajili ya michezo kwa sababu ni sera yetu ya mwaka 1995. Ahsante. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa mila na desturi za makabila yetu ya Tanzania zinaendelea kupotea kwa kasi kubwa; na kwa kuwa vijana wetu wameingia kwenye utandawazi wa kuiga mila za kigeni mpaka wanaiga mambo ambayo sio utamaduni wetu. Kwa mfano, kumekuwa na wimbi la vijana wa Tanzania kutaka mabadiliko ya ndoa za jinsia moja, mwanaume kwa mwanaume au mwanamke kwa mwanamke ambazo siyo desturi na mila zetu za Tanzania kama jinsi tunavyoishi na makabila yetu yalivyo. Je, ni lini Serikali itawatambua rasmi Machifu na Watemi ili waweze kutoa mchango wao kwenye jamii kurekebisha na kufundisha mila na desturi zetu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa mikoa mingi ya Tanzania haina nyumba za makumbusho za kuhifadhi hizo kanzidata za mila na desturi za makabila tofauti. Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za makumbusho kwenye mikoa yote ya Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Restituta Mbogo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ametaka kujua ni lini Serikali itawatambua rasmi Machifu pamoja na Watemi. Niseme kwamba si kwamba Serikali haiwatambui Machifu pamoja na Watemi ambao tunao na ndiyo maana katika shughuli mbalimbali ambazo zimekuwa zikifanywa na Serikali watu hawa wameendelea kualikwa ikiwepo shughuli ya Mwenge. Kwa hiyo, ni kwamba Serikali inawatambua na itazidi kuwatambua Machifu na Watemi kwa sababu ni njia mojawapo ya kuendelea kuenzi na kudumisha mila pamoja na tamaduni zetu.
Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka kujua kwamba ni lini Serikali itajenga maeneo ya makumbusho kwa ajili ya kuhifadhi mila na tamaduni. Kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi kwamba sisi kama Serikali ni waratibu pamoja na wasimamizi wa sera na sheria zinazohusiana na masuala mazima ya utamaduni, wamiliki wakubwa wa utamaduni ni jamii kwa maana ya wananchi. Kwa hiyo, ni jukumu letu sisi sote kuhakikisha kwamba tunashirikiana pamoja na Serikali kujenga na kudumisha mila na tamaduni za Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, pia kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi, nitoe wito kwa mashirika yote ya umma na ya kiserikali na watu binafsi kuhakikisha kwamba tunashirikiana kwa pamoja kudumisha mila pamoja na tamaduni ikiwepo suala ambalo ni muhimu sana la kujenga makumbusho kwa ajili ya kuhifadhi mila pamoja tamaduni zetu. Ahsante.

WAZIRI HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO:
Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kunipa fursa hii. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda tu niongeze kwamba wiki iliyopita nilipata bahati kubwa ya kuhudhuria Maadhimisho ya Kituo cha Kumbukumbu ya Utamaduni wa Kabila la Wasukuma huko Bujora, Mwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kilichonifurahisha sana ni ushiriki mkubwa wa Machifu wa Kisukuma, wote walikusanyika pale. Wana Umoja wao unaitwa Bubobatemi-Babusukuma. Waliweza hata kunipa cheo pale kuwa Manji Mkuu wa ngoma moja pale na ni cheo kikubwa sana hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nataka tu kusisitiza kwamba nafasi ya Machifu katika kudumisha utamaduni wa Tanzania tunaiona. Nadhani hili suala tutaendelea kuliangalia kwa umakini na kulileta lipate mjadala mpana tuweze kuiona nafasi yao kabisa ambayo itaweza kujikita hata kisheria.
Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kusema kwamba Waheshimiwa Wabunge wametoa mchango mkubwa sana katika hili eneo hasa tukizingatia ukuzaji wa utamaduni Mkoa wa Songea, Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya, Tamasha la Utalii Nyasa; Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, Majimaji Selebuka; Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson ambaye kila mwaka naye anaazimisha ngoma za kiutamaduni Mkoa wa Mbeya. Ningeoomba Waheshimiwa Wabunge wote tuingie katika kuhamasisha utamaduni katika maeneo yetu. (Makofi)
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona, naomba niulize swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Balozi wa Namibia alifanya ziara katika Tarafa ya Kwamtoro na kukutana na Wazee wa Kabila la Kisandawe. Moja kati ya maelezo yake ni kwamba lugha wanayoongea Wasandawe inafanana na lugha wanayoongea watu wa Kusini mwa Namibia halikadhalika na watu wa kabila la Xhosa kule Afrika ya Kusini. Alisema yuko tayari kuwachukua Wazee wa Kisandawe kwenda kule Namibia kwa ajili ya kutambuana na ndugu zao. Je, Serikali haioni kwamba upo umuhimu sasa wa kuangalia baadhi ya makabila ya Tanzania na makabila mengine Afrika ili kujenga mahusiano?
NAIBU WAZIRI HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Nkamia, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mkamia Serikali inaona kwamba kuna umuhimu mkubwa kwa sababu tunatambua kwamba lugha zote ambazo zipo hususani lugha za Kiafrika ni lugha za Kibantu ambazo zina mwingiliano mkubwa sana. kwa hiyo, sisi kama Serikali tunatambua kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuangalia hizi lugha ambazo zipo katika nchi yetu ya Tanzania namna ambavyo zinahusiana na lugha zingine ambazo zipo kwenye nchi zingine. Kwa hiyo, niseme kwamba wazo lake ni zuri na sisi kama Wizara tumelipokea na tunaahidi kwamba tutalifanyia kazi. Ahsante.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pia nashukuru kwa majibu mazuri sana ya Naibu Waziri na naipongeza Serikali kwa sababu imeendelea kuimarisha sana Sekta hii ya Sanaa, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa sasa Serikali inatambua umuhimu wa vijana kujiajiri kupitia sanaa; je, haioni sasa umefika wakati muafaka kuboresha vitengo vya Maafisa Utamaduni ambao kwa sasa hawana vitendea kazi. Ili waweze kuwapatia magari na fedha kwa ajili ya kuwafikia vijana hasa walioko vijijini na wenye vipaji?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa vijana wengi sasa wamejitokeza kuonesha ufundi stadi wao katika sanaa mbalimbali, lakini kuna uharamia mkubwa sana katika mitandao, kuna fedha nyingi zimebaki kule. Je, Serikali haioni sasa umefika wakati muafaka wa kurasimisha zile kompyuta ambazo zinatumika kuuza miziki ya Wasanii, ili Serikali yenyewe ipate mapato, lakini na Vijana waweze kupata mapato kupitia mitandao hiyo? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumpongeza kwa sababu amekuwa ni mpambanaji mkubwa sana ndani ya Bunge ya masuala yote ambayo yanahusu Sanaa pamoja na Wasanii.
Mheshimiwa Spika, sasa nikija katika swali lake ambalo ametaka kujua Serikali ina mpango gani katika kuboresha maslahi ya Maafisa Utamaduni Nchini. Nikiri kwamba sisi kama Serikali tunatambua kwamba, Maafisa Utamaduni nchini kote wanafanya kazi kwenye mazingira magumu. Hata hivyo, kwa sababu tunatambua pia kwamba sisi kama Wizara ya Habari, Maafisa Utamaduni wako kwenye Wizara ya Habari Kisera, lakini kiutendaji wanawajibika chini ya Wizara ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI, tutaendelea kushirikiana kuhakikisha kwamba tunaboresha, mazingira ya Maafisa Utamaduni nchini. Kama haitoshi nimhakikishie kwamba kwa sasa hivi, Wizara ipo katika hatua za mwisho kabisa za kuhuisha na kuboresha ile Sera yetu ya Utamaduni ya mwaka 1997 ili basi iweze kuendena na mazingira ya sasa.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, ameuliza kuhusiana na kurasimisha kompyuta ili kuweza kutunza haki za Wasanii. Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie kwamba, tunatambua kabisa kwamba kumekuwa na changamoto kubwa sana ya wizi wa kazi za sanaa. Sisi kama Serikali zipo jitihada mbalimbali ambazo tumezichukua katika kukabiliana na uharamia huo wa kazi za sanaa nchini. Si tu katika kurasimisha kompyuta, lakini kuna jitihada mbalimbali mojawapo ikiwa ni kutoa elimu kwa Wasanii wetu ili waweze kujua ni namna gani ya kuweza kuhifadhi kazi zao, lakini vile vile waweze kusimamia haki zao, kwa sababu changamoto kubwa imekuwa ni wao wanaingia mikataba ambayo haizingatii maslahi yao.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo kama Wizara tumefanya, ni kuhakikisha kwamba, sasa hivi tumeunda Kamati ambayo inapitia Mikataba yote ya Wasanii. Ni hivi juzi tu tumeshuhudia Waziri wangu Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe akilivalia njuga suala la Mzee Majuto kudhulumiwa haki yake na nimhakikishie kwamba kwa sasa hivi tumefika kwenye hatua nzuri. Kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba Kamati hiyo itakapokamilisha kupitia hiyo mikataba yote ya Wasanii nchini, Wasanii wataweza kunufaika na kazi zao.
Mheshimiwa Spika, kama haitoshi mwisho kabisa kwa sasa hivi, Wizara tuko katika kwenye mazungumzo na wenzetu wa Wizara ya Viwanda ili basi ile Idara ya COSOTA iweze kurudishwa kwenye Wizara ya Habari, Sanaa na Utamaduni.
Ili basi matatizo yote ambayo yanawahusu Wasanii yaweze kushughulikiwa na Wizara Moja. Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa changamoto kubwa inajitokeza kutokana na uhaba wa hawa Maafisa Utamaduni kwenye halmashauri zetu. Sasa Je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri Maafisa Utamaduni ili kuweza kukidhi haja ya Sanaa. Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba, hapo nyuma kulikuwa kuna changamoto kubwa sana ya Maafisa Utamaduni kwenye halmashauri zetu, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, halmashauri nyingi zilishaandika barua ya kuomba vibali kutoka Utumishi vya kuweza kuajiri Maafisa Utamaduni. Mpaka sasa hivi karibu halmashauri nyingi zina Maafisa Utamaduni.
Mheshimiwa Spika, kama haitoshi sisi kama Wizara, tunaendelea na mchakato wa kuonesha kwamba tunaajiri Maafisa Utamaduni wapya, hususani katika Mikoa na Halmashauri ambazo ni mpya. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tatizo hilo kwa kiasi kikubwa sana limeshashughulikiwa na Wizara yetu ya Habari, nadhani hata Waheshimiwa Wabunge mtakuwa mashahidi.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuwapongeza community redio ya Mashujaa FM kwa kufanya coverage kwa niaba ya TBC.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika bajeti ya mwaka 2016/2017 Serikali ilitenga hiyo bajeti ya kujenga mtambo Nangurukuru, mwaka 2017/2018 na hii 2018/2019 imerudia kuwa inaendelea kutenga bajeti bila ya utekelezaji. Sasa nini commitment ya Serikali katika bajeti ya mwaka huu kwa sababu inaonekana kana kwamba Serikali haina nia thabiti ya kujenga mtambo huo?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa TBC ndio chombo cha Taifa na kina jukumu la kutoa mawasiliano kwa wananchi, kutokana na kusua sua kwake Mheshimiwa Waziri haoni kwamba wanawakosesha haki wananchi wa Kilwa kupata habari? Lakini pia…
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ameonesha wasiwasi kwamba TBC inasuasua katika utekelezaji wa usikivu hususan katika Wilaya yake ya Kilwa. Kwanza napenda kutumia nafasi hii kumtoa hofu Mheshimiwa Mbunge kwa sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya kwanza, wote tunafahamu kwamba katika bajeti ya fedha ya mwaka WA 2017/2018 Serikali ilitenga shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kuboresha usikivu wa TBC na fedha hiyo ilishatolewa yote. Katika bajeti ya mwaka huu wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga bajeti ya shilingi bilioni tano. Kwa hiyo tuna imani kabisa fedha hiyo itatolewa yote kwa sababu imekuwa ni mpango wa Serikali na tumeona kabisa Serikali ina commitment na ndiyo maana katika fedha zote ambazo zinatengwa zimeendelea kutolewa kama inavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, kwamba TBC kusuasua kwake kunawakosesha haki wananchi, nimtoe hofu kama ambavyo tumejibu katika jibu letu la msingi, kwamba katika mwaka huu wa fedha wa 2018/2019 Serikali kupita shirika lake la TBC imejipanga kujenga mnara mpya wa kurushia matangazo yake katika eneo la Nangurukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaamini kabisa na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mimi kama Naibu Waziri pamoja na Waziri wangu tutawasimamia katika mwaka huu wa fedha kuhakikisha kwamba mtambo huo unajengwa, ili basi wananchi wa Kilwa waweze kupata haki yao ya kuweza kupata habari, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nitoe shukurani kwa Wizara hii kwa sababu wametujengea mtambo katika eneo letu la Kwemashai kule Lushoto; lakini bado usikivu haupo vizuri. Sasa, je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba usikivu wa TBC katika Wilaya ya Lushoto na leo wenyewe wapo hapa wamekuja kufuatilia jambo hili utakuwa na usikivu unaoeleweka?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Rashid Shangazi kwa sababu yeye amekuwa ni mdau mkubwa wa TBC ndani ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Hata hivyo, kama ambavyo ametoa pongezi na mimi kwa niaba ya Serikali napenda kupokea pongezi hizo, kwamba TBC sasa hivi tumekwisha kuweza kujenga Mtambo katika Wilaya yake ya Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ambayo ipo katika Wilaya hiyo ya Lushoto ambayo inasababisha usikivu kutokuwa mzuri ni kwamba mitambo hii inapofungwa lazima kuwe kuna muda kidogo wa kuweza kufanyia maboresho. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuweza kumhakikishia Mheshimiwa Shangazi, pamoja na wananchi wote wa Wilaya ya Lushoto ambao wapo ndani ya Bunge hili, kwamba ndani ya miezi miwili nilishaongea na Mkurugenzi wa TBC ameniahidi kwamba atatuma timu yake ya wataalam kwenda kufanya maboresho katika mtambo huo ili basi usikivu wa TBC uwe mzuri. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mkoa wa Katavi usikivu wa TBC sio mzuri kabisa na baadhi ya maeneo hawasikii matangazo ya aina yoyote na hutumia matangazo ya nchi jirani. Je, ni lini Serikali italeta mtambo kwenye Mkoa wa Katavi ili wananchi waweze kupata huduma ya TBC?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018 ipo mikoa mitano ambayo ipo kwenye bajeti. Mikoa hiyo ni mikoa mipya ukiwemo Mkoa wa Songwe, Mkoa wa Simiyu, Mkoa wa Katavi, Zanzibar pamoja na Mkoa wa Njombe. Kwa hiyo nichukue nafasi hii kuweza kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka huu wa fedha 2018/2019, Mkoa wa Katavi upo kwenye mpango na tunamhakikishia kwamba usikivu wa TBC katika Mkoa wake utaboreshwa. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ludewa kijiogrofia ni tambarare, milima na mabonde na kwa maeneo mengi inayosikika inasikika Redio Malawi. Je, ni lini TBC itasikika maeneo ya Ludewa yote?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimeshajibu kwamba, katika mwaka wa fedha 2018/2019 TBC imetengewa bajeti ya shilingi bilioni tano. Kati ya mikoa ambayo itashughulikiwa ni Mkoa wa Njombe. Kwa sababu natambua kabisa kwamba Wilaya ya Ludewa ipo ndani ya Mkoa wa Njombe, kwa hiyo, ni hakika kabisa kwamba TBC ndani ya mwaka huu wa fedha itaweza kusikika na maboresho makubwa yatafanyika katika Wilaya hiyo ya Ludewa pamoja na Mkoa mzima wa Njombe.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali langu nililomwuliza, ni kiasi gani cha mgawo wa fedha hizi za FIFA wamewahi kuipatia Zanzibar? Jibu lake, anakuja kusema kwamba kuanzia mwaka huu tutapata 1.25. Kwa hiyo, amekwepa kabisa kunijibu swali langu nililomwuliza. Nataka kujua: Je, mmewahi kuipatia mgawo wowote Zanzibar kutokana na misaada hii inayotoka FIFA?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Nataka nijue, kwa kuwa TFF siyo chombo cha Muungano, Mheshimiwa Waziri wa Michezo sio Waziri wa Muungano na Wizara ya Michezo siyo Wizara ya Muungano; kwa hiyo, anaposema sasa kwamba kuanzia msaada huu unaokuja, mgawo utaenda kwa ZFA na TFF, nataka nijue, mtatumia formula ipi wakati mkijua kwamba masuala ya michezo Zanzibar wana Wizara yao na Tanzania Bara wana Wizara yao: Je, hamwoni hapa kwamba kuna mkorogano ambao kwa miaka yote na ndio maana Zanzibar tunakosa msaada huu wa FIFA?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikianza na swali lake la kwanza, ametaka kujua kwamba, ni kiasi gani? TFF imekuwa ikitoa misaada mbalimbali kwa Chama cha ZFA ambacho ni cha Zanzibar. Moja ya miradi ambayo tayari imeshapelekwa ZFA ni ujenzi na ukarabati wa Uwanja wa Gombani ambao uko Pemba. Kwa hiyo, siyo kweli kwamba TFF imekuwa haipeleki msaada Zanzibar, hapana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili ambapo ameelezea kwamba suala la michezo siyo la Muungano, nadhani Mheshimiwa Mbunge alikuwa hajaelewa jibu langu la msingi ambalo nimelitoa. Ni kwamba, ZFA ni sehemu ya TFF. Kwa tafsiri hiyo basi, maana yake fedha ambazo zinaletwa TFF zinagawiwa kwa mashirikisho yote ikiwepo ZFA ya Zanzibar, lakini si kwamba, ZFA inaletewa fungu lake peke yake, hapana, kwa sababu, ZFA siyo mwanachama wa CAF, lakini ZFA vilevile siyo mwanachama wa FIFA. ZFA iko chini ya TFF.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kabla sijauliza maswali yangu mawili ya nyongeza, ningependa tu niishauri Serikali pale ambapo Waheshimiwa Wabunge wanafanya mambo yanayoacha alama katika jamii watambuliwe. Uwanja wa Jakaya Mrisho Kikwete Youth Park ilikuwa ni kazi nzuri iliyofanywa na Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu. Mambo kama haya yakitajwa, kama Mheshimiwa Lema alivyojenga ile hospitali ya Mama na Mtoto kule Arusha, yanawatia moyo Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo wanaendelea kuhangaika kwa ajili ya kuwatumikia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hilo niombe kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo viwanja vingi sana vya michezo ambavyo vimevamiwa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Je, Wizara iko tayari kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, ili kurejesha viwanja hivi na kujenga viwanja vidogo vidogo kama huu wa Jakaya Mrisho Kikwete Youth Park kwa ajili ya michezo ya watoto wetu ambao wanacheza hovyo barabarani na kuhatarisha maisha yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna viwanja vya mpira wa miguu hapa nchini, ambavyo kwa kweli ni vibovu. Hivi karibuni timu ya Yanga ilicheza kwenye uwanja fulani, sitaki niuseme na ilipata shida sana kwa kweli, yaani unaona hata wanavyopasiana wanavyopiga chenga na nini inaathiri matokeo. Sasa kwa nini viwanja kama hivi visifungwe ile michezo ya ligi TFF ikahamishia kwenye viwanja vya karibu ili kutoa nafasi viwanja kwa hivyo kukarabatiwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa maswali yake mazuri ambayo ameyauliza, lakini niseme kwamba ushauri ambao ameutoa tumeupokea na tutaendelea kuufanyia kazi. Nikianza na swali lake la kwanza ambalo amezungumzia viwanja kuvamiwa. Nikiri kwamba ni kweli kuna tatizo kubwa sana la viwanja kuvamiwa nchini Tanzania na hata juzi ambapo nilikuwa Mkoa wa Kigoma, Wilaya ya Kibondo nilikuta kwamba kuna kiwanja kizuri kabisa cha mpira lakini kimevamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho naweza kusema ni kwamba, changamoto kubwa ambayo inasababisha viwanja hivi kuweza kuvamiwa ni kwa sababu kwanza viwanja vinakua havina Hati Miliki, hilo la kwanza, lakini unakuta viwanja vipo lakini havijazungushiwa wigo. Kwa hiyo nitumie nafasi hii kuweza kutoa wito kwa wamiliki wa hivyo viwanja, iwe ni Halmashauri, kampuni za watu binafsi au vyama vya kisiasa kuhakikisha kwamba cha kwanza, wanavitafutia Hati hivyo viwanja lakini jambo la pili waweze kuzungushia wigo hivyo viwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake pili ameuliza kuhusu ubovu wa viwanja na ameshauri kwamba kwa nini hivyo viwanja visifungwe ili ukarabati uweze kufanyika. Niseme kwamba ushauri wa Mheshimiwa Mbunge tumeupokea, lakini kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi kwamba suala la ukarabati wa viwanja si suala la Serikali peke yake, ni suala la Serikali lakini kushirikiana na wadau wote ambao wanamiliki viwanja hivyo. Kwa hiyo nitumie fursa hii pia kwa wadau wote ambao wanamiliki hivyo viwanja kuhakikisha kwamba wanatenga fedha, lakini vilevile wanashirikiriana na TFF kuhakikisha kwamba hivyo viwanja vinaweza kukarabatiwa ili basi wanamichezo wetu waweze kucheza michezo vizuri.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nami nianze tu kwanza kwa kuishukuru Wizara kwa kuendelea na jitihada za kuboresha na kuimarisha Uwanja wa Nyamagana. Sasa kwa sababu tunaamini kwamba ili tuwe na vijana wengi ambao wanacheza mpira vizuri ni lazima tuwe na viwanja vingi kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wanasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Jiji la Mwanza tuna Milongo Sports Center ina viwanja takribani vitano kwa wakati mmoja. Ningependa sasa kumwomba Mheshimiwa Waziri apate nafasi aje atembelee viwanja hivi na tuone namna ya kuviboresha ili kupata vijana wengi zaidi; je, yuko tayari kufanya hivyo tukimaliza Bunge hili?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mabula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza Wabunge wote wa Jiji la Mwanza kwa jitihada kubwa sana na nzuri ambazo wanafanya katika kuboresha viwanja vyetu. Vilevile niseme kwamba ni juzi tu nilikuwa Wilaya ya Nyamagana na nikatembelea ule Uwanja wa Nyamagana ambao umekarabatiwa kwa jitihada za Halmashauri, Waheshimiwa Wabunge, pamoja na wadau. Niseme kwamba ombi lako nimelipokea na nitafika tena kwenye Jiji la Mwanza ili kuweza kuangalia namna gani ambavyo tutashirikiana pamoja. Ahsante.
MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) wametupa upendeleo Jiji la Tanga kutaka kutujengea Uwanja wa kisasa, lakini cha kushangaza eneo lile halijazungushiwa uzio na watu wameshaanza kulivamia, sasa Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, je, ni lini harakati angalau za kuanza maandalizi na kujenga uzio katika lile eneo ili lisivamiwe utaanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Jiji la Tanga ni eneo ambalo limetengwa kwa ajili ya kujenga uwanja changamani wa michezo kwa fedha ambazo tunategemea zitatoka FIFA. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba as soon as fedha hizo zitakuwa zimefika, ujenzi wa uwanja huo utaanza. Kwa hiyo, nimtoe shaka kwamba, ujenzi utaanza mapema sana mara tu fedha zitakapokuwa zimefika. Ahsante.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Asilimia 90 ya wanariadha wanatokea Mkoa wa Manyara, lakini pia wapo wengi na taarifa iliyosomwa hapo na Naibu Waziri ni kuanzia miaka ya tisini kurudi nyuma, wapo wengi, akina John Yuda Msuri, Fabian Joseph, Andrew Sambu Sipe; wote hawa rekodi zao hazijavunjwa mpaka sasa kwa kuwa walikuwa wameshiriki mbio mbalimbali za kimataifa. Swali langu la msingi lilisema; ni lini utaratibu wa kuwaenzi wanariadha hawa utafanyiwa kazi sasa? Muda mfupi uliopita tulizungumza habari hapa na Waziri wa TAMISEMI alijibu suala la Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanaofanya vizuri kuwa recognized na kupewa vyeti, habari gani kwa ajili ya wanariadha hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, amejibu hapa Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba picha zao zitawekwa kwenye jumba la makumbusho, je, hiyo inatosha? Wapo wanariadha wengi ambao hali zao za kimaisha ni duni, naomba kujua wanafanyiwa lini mchakato wa kutambuliwa juhudi zao. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie nafasi hii kuweza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa ni mfuatiliaji mzuri sana wa masuala ya michezo. Nikianza na swali lake la kwanza, ni kweli kwamba sisi kama Wizara tunatambua kwamba wapo wanariadha wengi sana ambao wanatoka kwenye Mkoa wa Manyara kama ambavyo yeye mwenyewe amewataja, lakini sisi kama Serikali hatuwezi kuangalia tu mkoa mmoja, ni wanariadha wengi ambao wanatoka maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi kwamba sisi kama Serikali tunao mpango wa kuanzisha makumbusho rasmi kwa ajili ya kuweka kumbukumbu zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua sasa hivi sisi kama Wizara tunayo ile kampeni yetu ya uzalendo ambayo kila mwaka tumekuwa tukiifanya na kitu ambacho tunafanya ni kuweza kuwaenzi watu mbalimbali ambao wameliletea heshima kubwa Taifa hili. Mwaka jana nakumbuka tulianza kwa wanamuziki lakini mwaka huu tutajipanga kuangalia namna gani ambavyo tunaweza tukawaenzi wanariadha wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niulize swali la wanariadha ambao nao Mkoa wa Singida ni miongoni mwa mikoa ambayo ilikuwa inafanya vizuri sana katika riadha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jimbo ninalotoka mimi kulikuwa na wanariadha miaka ya nyuma, lakini hata mimi mwenyewe nilikuwa mwanariadha. Kwa kuwa ili wanariadha na vijana ambao wapo shuleni waweze kupata hamasa ya michezo ni pamoja na vyombo vya habari ikiwemo TBC kusikika katika maeneo mbalimbali. Je, ni lini sasa Serikali itafanya TBC isikike katika eneo la Itigi ambapo haisikiki kabisa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie fursa hii kuweza kumpongeza Mheshimiwa Massare kwa sababu swali lake la usikivu wa TBC amekuwa akiuliza karibu kila Bunge, lakini niseme kwamba ni suala la kibajeti na kwa kuwa hili ni Bunge la Bajeti kwa mwaka huu tutaangalia namna gani ambavyo tutaboresha usikivu katika eneo lake la Itigi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Natambua juhudi kubwa anayofanya Naibu Waziri. Michezo ni sekta muhimu, lakini pamoja na hivyo, vyuo vyetu vikuu havina vipaumbele vya miundombinu ya viwanja. Mfano mzuri ni mwaka jana, tulikuwa na mashindano ya vyuo vikuu vya Afrika Mashariki, tulikuwa na michezo...

MWENYEKITI: Uliza swali tu Mheshimiwa.

MHE. ANNA J. GIDARYA: …kulikuwa na michezo kumi na tisa, Tanzania tulishiriki michezo tisa tu jambo ambalo
limesababisha nchi yetu kukosa vikombe vingi. Je, ni lini sasa Serikali itaboresha miundombinu na kuipa michezo kipaumbele katika vyuo vyetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuweza kumpongeza Mheshimiwa Anna kwa sababu kwanza ni mwanamichezo mahiri, lakini vilevile ni Kiongozi wa CHANETA Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye swali lake la msingi, ametaka kujua kwamba ni lini sasa Serikali itaweza kuboresha viwanja vya michezo, hususan kwenye vyuo vikuu. Nikiri kwamba ni kweli mwaka jana tulikuwa tuna mashindano na yeye mwenyewe pia alishiriki, pamoja na kwamba tuna uhaba wa viwanja vya michezo, lakini kama ambavyo tumekuwa tukisema kwamba Sera yetu ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 inasisitiza kwamba suala la michezo sio suala la Serikali peke yake, ni suala la Serikali lakini vilevile tuweze kushirikiana pamoja na wadau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuweza kuwaambia na kuwaomba Wabunge wote kuiga mfano wa Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu kwa namna ambavyo amefanya maboresho ya kiwanja kule Lindi. Kwa hiyo suala hili la michezo sio suala la kuiachia Serikali peke yake, tuendelee kushirikiana pamoja na Serikali na sisi kama Wizara tuko tayari kuendelea kutoa utaalam pamoja na mafunzo mbalimbali namna gani ya kuweza kuboresha hivyo viwanja.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa majibu mazuri ambayo tumeyapata. Pamoja na majibu hayo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, tunaipongeza Serikali kwa uamuzi wa kujenga Kituo Kikuu cha Kumbukumbu Wilayani Kongwa kwa sababu Kongwa ina historia ya wapigania uhuru. Je, kituo hicho kitaanza kujengwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa ushirikishwaji wa wadau huharakisha shughuli za maendeleo na nimeona katika Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wadau wameshirikishwa, Wachina wamejenga majengo mazuri na makubwa pale chuo kikuu Dar es Salaam. Je, Serikali ina mpango wowote wa kushirikisha wadau ili jengo hilo likamike katika uongozi wa Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Felister Bura kwa niaba ya Mheshimiwa Livingstone Lusinde kwa maswali yake mazuri ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilianza na kwanza ameanza kwa kutoa pongezi kwa Wizara, tumepokea pongezi hizo. Vile vile swali lake la msingi la kwanza ametaka kujua, je, ni lini kituo hicho kitaanza kujengwa rasmi. Tayari ujenzi wa hiyo kituo ulishaanza na tulishaanza tangu mwaka 2015 ambapo ukarabati wa hicho kituo ulianza. Hata hivyo, kwa sababu ni suala la kibajeti na kwenye bajeti yetu ya mwaka jana kuna fedha ambayo ilitengwa kwa ajili ya kwenda kukarabati kituo hicho. Kwa hiyo, naomba nichukue nafasi hii kuweza kumhakikishia Mheshimiwa Bura kwamba ukarabati wa hicho kituo na kuweka miundombinu mingine unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kwa sababu lengo la Wizara ni kuhakikisha kwamba hicho kituo kinakuwa pia center kwa ajili ya masuala mazima ya utalii. Kwa hiyo mipango ambayo ipo pale ni mikubwa mpango mmojawapo ni kuhakikisha kwamba tunajenga kituo cha ndege lakini vilevile tuweze kujenga hotel za five stars pale ili kiweze kuwa kituo kikubwa cha masuala ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake pili ametaka kujua kwamba kuhusiana na kuweza kushirikisha wadau. Kama ambayo nimejibu kwenye jibu langu la msingi ni kwamba sisi kama Wizara suala hili hatufanyi peke yetu tumekuwa tukishirikiana na wadau. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuweza kuwahamsisha wadau mbalimbali waweze kushiriki katika kuhakikisha kwamba tunatunza hizi kumbukumbu za Mwalimu Nyerere. Ahsante.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la dogo nyongeza. Kwa kuwa Serikali imetamka Vituo vya Kumbukumbu ya Baba wa Taifa na kadhalika, lakini Mkoa wa Tabora una historia kubwa, nilitegemea kwamba leo Mheshimiwa Waziri atatamka kwamba Tabora nayo iwemo katika orodha ya Kumbukumbu ya Baba wa Taifa. Nasema hivi kwa sababu uhuru na maelekezo mengine yote ya Baba wa Taifa yalitoka Mkoa wa Tabora, karata tatu zimetoka Mkoa wa Tabora. Baba Taifa ameacha historia kubwa katika Mkoa wa Tabora kwa kusoma na kadhalika.

Kwa hiyo, kwa kutokuweka orodha ya Kituo cha Tabora kukitambua rasmi kwa kweli hawautendei haki Mkoa wa Tabora. Je, ni lini sasa Serikali itaingiza katika orodha ya Kumbukumbu ya Baba wa Taifa kwenye vituo hivyo ambacho vimetamkwa hivi leo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Mwanne Nchemba, mama yangu kwa maswali ya nyongeza. Napenda nitumie fursa hii kumhakikishia kwamba kwa suala hili la uhifadhi wa Kumbukumbu za Mwalimu Nyerere kitu ambacho kama Wizara tunafanya, kwa sababu tulitaka tufanye katika mapana makubwa, tunayo sasa hivi Programu yetu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika.

Kwa hiyo, kupitia hiyo pragram Mkoa wa Tabora ni mkoa mmojawapo kati ya mikoa 15 ambayo imeteuliwa na Wizara ili kuweza kuyabaini yale maeneo maalum ambayo yallitumika katika ukombozi wa Bara la Afrika. Kwa hiyo Mkoa wa Tabora upo, lakini ni katika ile Program kubwa ya Ukombozi wa Bara la Afrika. Ahsante.
MHE. MAULID S. MTULIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nitoe shukrani zangu za dhati kwa majibu mazuri ya Serikali. Vilevile niendelee kuhimiza Serikali kwamba mabadiliko ya Sera na Sheria ya Bodi ya Filamu yafanyike kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa wasanii wetu wamedhulumiwa kazi zao na wasambazaji walikuwa wanawaingiza mikataba kama wasimamizi badala ya wamiliki wa kazi; kwa kuwa sheria ipo kulinda haki za wasanii; na kwa kuwa nchi za wenzetu mfano Nigeria iliwahi kutoa tamko kuhakikisha kazi zote za wasani umiliki urudishwe kwa wasanii wenyewe, je, Serikali yetu ya Tanzania iko tayari sasa kutoa tamko kuhakikisha wale wote waliodhulumu kazi za wasanii umiliki unarudi kwa wasani wenyewe ili waweze kunufanika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wasanii wetu wanaendelea kuzalisha kazi nzuri kabisa; na kwa kuwa walaji wengi katika jamii wanahitaji kuendelea kuziona kazi za wasanii na katikati yake kuna ombwe kubwa kwamba wasanii, waandaaji na walaji hawaonani, je, Serikali ipo tayari kuja na suluhisho kuhakikisha kazi za wasanii zinafika kwa walaji ili wasanii waepukane na kutembeza CD mkononi wao wenyewe?
NAIBU WAZIRI WA HABARI UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Said Mtulia, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kwa jinsi ambavyo amekuwa akipambania maslahi ya wananchi wa Kinondoni, ukizingatia kwamba wasanii wengi walioko katika jiji la Dar es Salaam wanaishi katika Wilaya yake ya Kinondoni. Kwa hiyo, nampongeza sana kwa kupambania maslahi ya wasanii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali lake la kwanza ambapo ametaka kujua kama Serikali tuna mpango gani wa kurejesha zile hakimiliki ambazo zimechukuliwa kutoka kwa wasanii. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi kwamba kwa Sheria ya Hakimiliki ya mwaka 1999 ambayo tunayo sasa hivi inatoa haki na uhuru kwa msanii mwenyewe kuamua ni namna gani ambavyo atataka kuuza haki yake. Kama akitaka kuuza kazi zake zote kwa maana kwamba anauza pamoja na ile master ya kazi yake au kuuza baadhi kazi zake. Kwa hiyo, ni suala la msanii mwenyewe kuamua anataka kuuza kazi zake kwa njia gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi kama Serikali kwa kutambua kwamba suala hilo limeleta mchanganyiko mkubwa sana na halina maslahi kwa wasanii, kitu ambacho tunafanya kwanza ni kutoa elimu kwa wasanii kuweza kutambua haki na thamani ya kazi zao, kwa sababu tumeona madhara makubwa sana ambayo yamekuwa yakiwapata wasanii pale ambapo wanauza mpaka umiliki wa zile kazi zao. Kwa hiyo, tunaelimisha wasanii kwanza waweze kutambua kwamba kazi zao zina thamani, ukiuza leo kazi yako pamoja na master ni kitu ambacho kitaendelea kutumika miaka mingi matokeo yake hayatakuwa mazuri kwa miaka ijayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaendelea kutoa wito kwa wasanii wote nchini Tanzania kwanza kutambua thamani ya kazi yao na kuona kwamba siyo jambo jema kuuza mpaka umiliki wa kazi zao. Hata hivyo, kwa sheria ambayo tunayo inatoa haki kwa msanii kuamua ni namna gani ambavyo atauza kazi yake. Kwa hiyo, sisi kama Serikali hatuwezi kutoa kauli ya moja kwa moja kwa sababu sheria imewapa uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija kwenye swali lake la pili ambalo amezungumzia kuhusu tatizo la usambazaji, ni kweli kwamba kwa miaka ya hivi karibuni tasnia yetu ya sanaa imekumbwa na changamoto nyingi ikiwepo suala la usambazaji. Kama ambavyo tunajua tatizo la usambazaji kwa miaka ya hivi karibuni lilisababishwa na kukosekana kwa kazi ambazo zina ubora na ubunifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usambazaji ni biashara kama biashara zingine. Kwa hiyo, sisi kama Wizara tunaamini kwamba hakuna mfanyabiashara atawekeza mtaji wake kwenye biashara ambayo anaamini kwamba haiwezi kumpa faida hapo baadaye. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tunaendelea kutoa wito kwa wasanii kwanza kutengeneza kazi ambazo zina ubora na zitaleta ushindani kwenye soko lakini zitavutia wasambazaji wengi kuja kuwekeza mitaji kwenye kazi zao hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa sababu tunajua kwamba sasa hivi pia kuna mabadiliko ya sayansi na teknolojia na tumeshuhudia wasanii wengi sana wamehama kutoka kwenye mfumo wa kusambaza kazi zao kwa njia ya CD wanatumia njia ya mtandao. Kuna msanii anaitwa Wema Sepetu, kwenye filamu yake ya Heaven Sent. amefanya vizuri sana, amesambaza kazi yake kwa njia ya mtandao na mauzo yamekuwa mazuri. Kwa hiyo, nitoe wito kwa wasanii sasa waangalie namna gani ambavyo wataenda mbele zaidi kwa mabadiliko haya ya sayansi na teknolojia ili waanze kusambaza kazi zao kwa njia ya kimtandao.
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasanii wa Tanzania changamoto yao kubwa sana na namba moja ambayo inawakabili ni wizi wa kazi zao. Tumekuwa tukiona kazi zao zikiuzwa kwa holela kwenye maeneo mbalimbali lakini Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki, Na.7 ya mwaka 1999 imeonekana kuwa haina meno wala haiwasaidii wasani wa Tanzania. Je, ni lini Serikali italeta sheria hii hapa Bungeni ili tuweze kuifanyia mabadiliko ili wasanii wa Tanzania ambao wanaleta sifa kubwa kwa Tanzania kwa kupitia sanaa yao waweze kufaidika na kazi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Profesa Jay kwa swali nzuri la nyongeza kwa sababu yeye pia ni msanii, kwa hiyo, anatambua changamoto ambazo zinawakumba wasanii nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna changamoto kubwa sana ya suala la wizi ya kazi za sanaa, lakini sisi kama Wizara tumechukua hatua kadhaa. Hatua mojawapo ni kuhakikisha kwamba tunawahamasisha wasanii waweze kusajili kazi yao COSOTA ili pale ambapo wanapata matatizo iwe rahisi kuweza kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile amezungumzia changamoto kubwa ya sheria, tukiri kwamba hii sheria ina upungufu lakini Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ipo kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara, kwa hiyo, kama Wizara ambacho tunafanya sasa hivi ni kuhakikisha kwamba kitengo hiki cha COSOTA kinahama kutoka Viwanda na Biashara kuja kwenye Wizara yetu ya Habari ili tuangalie ni namna gani ambavyo tutaifanyia marekebisho sheria hii. Ahsante.
MHE. MGENI JADI KADIKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu yake lakini bado nina maswali mawili ya kumuuliza. Swali la kwanza; kwa kuwa vijana wengi au vijana wetu wadogo wanatumia mitandao kwa kutumia simu au ku-chart au kuangalia picha za ngono ambazo kuwa huleta hisia mbalimbali. Watoto hao ndiyo wale wanaobeba ujauzito wakiwa na umri mdogo kati ya darasa la sita mpaka darasa la tatu. Je, Serikali inaonaje suala hili?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; ziko nhi za wenzetu wanazuia mitandao kurusha picha za chafu. Je, Serikali yetu inashindwa nini baada ya kukemea na kudhibiti ili kuzuia mambo haya yasiendelee na wale watakaofanya hivyo wachukuliwe hatua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ambayo yameulizwa na Mheshimiwa Mgeni:-

Mheshimiwa Spika, nikianza na swali lake la kwanza ambalo ametaka kujua kwamba kwa upande wa Serikali tunaonaje masuala haya ya utandawazi. Ni kweli tunatambua kwamba, changamoto imekuwa kubwa sana kwa suala zima la maadili na kwa kiasi kikubwa sana inchangiwa na hii mitandao ya kijamii. Ndiyo maana kwa kujua hilo sasa sisi kama Serikali tulikuja na Sheria mbalimbali na Wabunge wa Bunge hili ndiyo ambao walizipitisha hizo Sheria, lengo ni kuhakikisha kwamba, tunawazuia watoto wetu hususan vijana ambao wako chini ya umri wa miaka 18 kuweza kujihusisha na vitu ambavyo havifai kwa Taifa letu. Kwa hiyo, kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi kwamba jukumu hili siyo jukumu la Serikali peke yake ni jukumu letu sote.

Mheshimiwa Spika, pia katika swali la pili, ametaka kujua kwamba nchi zingine zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana kuweza kudhibiti vijana wadogo ambao wako chini ya miaka 18 kuangalia vitu ambavyo havifai kwenye mitandao. Bado jibu langu liko pale pale kwamba ni wajibu wetu sote, upande wa Serikali na naweza nikasema kwamba kwa upande wa Serikali tumefanya kazi kubwa sana na ziko sheria ambazo tayari tumeshazipitisha ndani ya hili Bunge, lakini changamoto zimekuwa kubwa kwamba sheria hizi zinapopita Waheshimiwa Wabunge tumekuwa na ile tabia ya kuwa na mgawanyiko.

Mheshimiwa Spika, unakuta sheria tumepitisha kwa mfano, Sheria ya Cybercrime, lakini sasa unakuta wengine wanaanza kulalamika kwamba ile sheria inaminya uhuru na inakandamiza, kitu ambacho kinakuwa siyo cha kweli. Kwa hiyo nitoe wito ndani ya hili Bunge kwamba sheria kama hizi zinapopita katika Bunge ni vyema sisi kama viongozi tukawa wa kwanza kuzisimamia, lakini vilevile kwa yale maeneo ambayo sisi tunatoka, tuhamasishe jamii kuona kwamba namna gani ambapo suala zima la malezi siyo suala la Serikali peke yake ni suala la Serikali lakini pamoja na jamii kwa ujumla. Ahsante.
MHE. MAULID S. MTULIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali madogo mawili ya nongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, hivi sasa kuna mwamko mkubwa sana Nchini Tanzania kwa wazazi kutaka watoto wao washiriki kwenye michezo hasa ikichagizwa na mafanikio aliyoyapata kijana wetu Mbwana Samatta kucheza katika ligi ya Uingereza na mimi sasa hivi timu yangu ni Aston Villa, lakini kuna tatizo kubwa la vifaa vya michezo kwa wananchi wetu ili kuweza kushiriki vizuri michezo.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha vifaa vya michezo yote Tanzania vinapatikana kwa urahisi ili wazazi wachochee mchakato huu wa kuwa na wana michezo wengi Nchini Tanzania?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Wizara imesema suala la ujenzi wa viwanja ni la wadau na halmashauri na Halmashauri ya Kinondoni imeitikia wito huo kwa kuja na ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu pale Mwenge na vilevile kuna mchakato wa kujenga kituo cha malezi ya watoto ili tupate wachezaji bora kabisa. Serikali inatoa kauli gani kusaidia juhudi hizi ili wanaoonesha nia ya kuleta mabadiliko ya soka wapate kusaidiwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kwa sababu amekuwa ni mdau mkubwa sana wa masuala ya michezo, lakini nadhani hiyo inatokana na kwamba Jimbo lake ni Jimbo ambalo lina wanamichezo wengi pamoja na wasanii wengi. Kwa hiyo naamini kwamba Mheshimiwa Mbunge anafanya kazi nzuri sana na wananchi wake wanajivunia hilo.

Mheshimiwa Spoika, nikija sasa kwenye maswali yake mawili ya nyongeza; swali lake la kwanza amezungumza kwamba ipo changamoto ya vifaa vya michezo; na mimi nikiri kwamba ni kweli kumekuwepo na changamoto ya vifaa vya michezo, lakini kama Serikali hatujakaa kimya na tunayo Sera yetu ya Michezo ya Mwaka 1995 ambayo inazungumza kwamba suala zima la ujenzi wa viwanja pamoja na miundoimbinu yote ya michezo ni suala la Serikali lakini vilevile kwa kushirikiana na wadau.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa upande wetu sisi kama Serikali sasa hivi kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara tumekuwa tukihamasisha sana wafanyabiashara mbalimbali waendelee kuagiza vifaa vya michezo kutoka nje. Kama hiyo haitoshi kama Wizara vilevile kwa kupitia Sera yetu ya Awamu ya Tano ambayo ni Sera ya Viwanda tumekuwa pia tukihamasisha sana wawekezaji wa ndani pamoja na wawekezaji wa nje kuanzisha viwanda vya vifaa vya michezo kwa sababu tunatambua pamoja na kwamba vifaa vinakuwa ni adimu lakini pia changamoto kubwa imekuwa ni masuala ya kodi. Kwa hiyo hakuna namna nyingine ambayo tunaweza tukafanya kuondokana na tatizo hili, ni lazima sisi kama nchi tuhakikishe kwamba tuna viwanda ambavyo vinahusiana na uchakataji wa hivi vifaa vya michezo. Kwa hiyo, mikakati ipo na sisi kama Wizara tunaisimamia hiyo mikakati na tunamwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, tatizo hili kwa kadri miaka inavyozidi kwenda tunaendelea kulifanyia utatuzi.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili amezungumza namna gani ambavyo Halmashauri ya Kinondoni imeonesha jitihad. Nikiri kwamba ni kweli Halmashauri ya Kiondoni imekuwa ni mfano katika kuweka miundombinu ya michezo na natambua kwamba pia Halmashauri hiyo sasa hivi inamiliki timu ya KCMC, kwa hiyo ni namna gani ambavyo wanaonesha kwamba wana jitihada kubwa ya kukuza sekta hii ya michezo. Kwa hiyo, niseme sisi kama Wizara kwa kupitia TFF tumekuwa tukiunga mkono jitihada kama hizi za wadau kwa kuwapatia vifaa mbalimbali pamoja na nyasi na vifaa vingine na hayo tayari yameshafanyika kwenye baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana pia na Halmashauri ya Kionondoni wapeleke maombi TFF ili waone ni namna gani ambavyo wataweza kusaidia hivyo vifaa ili huo uwanja uweze kukamilika na nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, sisi kama Wizara tutakuwa pamoja naye kuhakikisha kwamba uwanja huo unakamilika, lakini vilevile support ya Serikali kupitia TFF iweze kuonekana. Ahsante sana.
MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza swali moja la nyongeza. Utamaduni una maana pana ikiwemo mazishi na mavazi. Je, ni lini Serikali itatangaza rasmi vazi la Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuridhika na majibu ambayo yametolewa na Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na swali lake la msingi ambapo ametaka kujua ni lini sasa Serikali itakuja rasmi na mchakato wa kutangaza vazi rasmi la Taifa, mara nyingi tumekuwa tukijibu swali hili ndani ya Bunge na sisi kama Wizara ambao ndiyo tunasimamia masuala mazima ya utamaduni ikiwemo lugha pamoja na vazi la Taifa, tupo kwenye mchakato wa kuhakikisha kwamba tunaleta vazi la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato unaoendelea sasa hivi ndani ya Wizara ni kuhakikisha kwamba tunakusanya mavazi yote kutoka kwenye mikoa kwa sababu tunajua kabisa vazi la Taifa siyo kitu ambacho tunaweza kukipata kutoka kwenye jamii moja. Tunachotaka kukifanya sasa hivi ni kuhakikisha mikoa na wilaya zote na wadau wote wa sanaa pamoja na wabunifu wa mavazi wanashiriki kwenye mchakato huu wa kupata vazi la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba pindi mchakato huo utakapokamilika sisi kama Wizara tutakuja rasmi na vazi la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali hata hivyo bado kuna changamoto mbili, tatu. Kwa mfano, madaktari wote wanaojitambulisha kama madaktari wa timu wanapokwenda na timu uwanjani, wengi siyo madaktari ni mashabiki tu ambao wanebeba hiyo mikoba ya first aid na hii ni hatari kwamba inapotokea matatizo wanakuwa hawana utalaam wa kutoa huduma ya kwanza viwanjani. Je, Serikali itakuwa tayari kuwashauri sasa TFF na Bodi ya Ligi kuwatambua madaktari wenye sifa ndiyo wapewe hiyo nafasi ya udaktari wa kuingia na timu viwanjani? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wachezaji wengi hawana bima za afya jambo ambalo linapelekea wanashindwa kujituma mazoezini na viwanjani kwa kuhofia kuumia. Serikali itakuwa tayari kuwashauri pia TFF badala ya kupoteza muda mwingi kuchunguza Makocha wamevaa nini sasa wakaongee na mashirika ya bima za afya ili waweze kuwapa bima za afya wachezaji?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa ni mdau mkubwa sana wa michezo na hivi majuzi


tumeshuhudia timu yake ya Umoja wa Vijana wa Temeke ikishinda kwenye Mashindano ya Ndondo Cup kwa msimu wa mwaka 2019. Kwa hiyo, hongera sana Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye maswali yake mawili ya msingi amezungumzia suala zima la madaktari wa timu kwamba wengi wa madaktari wa timu hawana vigezo au sifa za kuwa madaktari. Suala la timu zote kuwa na madaktari ni takwa la kikanuni. Nitumie fursa hii kwanza kuwataka wasimamizi wote wa vilabu nchini Tanzania kuhakikisha kwamba wanatumia madaktari ambao wana sifa za kuwa madaktari kwa sababu tunajua kwamba yako matatizo mbalimbali ambayo huwa yanawapata wachezaji pindi wanapokuwa kwenye mazoezi na kwenye michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Mbunge ametaka tuwashauri TFF wanatambua na kuhakikisha kwamba vilabu vyote vinakuwa na madaktari ambao wana sifa. Nitumie fursa hii kuwataka TFF kuhakikisha kwamba suala hili kwa sababu ni takwa la kikanuni na kikatiba ni vyema wakasimamia kuhakikisha kwamba vilabu vyote vinakuwa na madaktari wenye sifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la pili ametaka kujua kuhusiana na bima za afya. Suala la afya za wachezaji sisi kama Wizara tunalisimamia na ndiyo maana kwenye mashindano yote tunahakikisha kwamba kabla wachezaji hawajaenda kwenye mashindano wanapima afya zao. Mheshimiwa Mbunge ametaka kujua kwamba kwa nini sisi kama Serikali tusiwashauri TFF waongee na mashirika ya bima za afya ili wachezaji waweze kupatiwa bima za afya, ushauri huu mzuri na sisi kama Wizara tumeupokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba TFF wameuchukua na wataufanyia kazi kwa sababu ni takwa la kikanuni na kikatiba kuhakikisha kwamba wachezaji wote wanakuwa na bima za afya. Suala la bima ya afya siyo tu wachezaji peke yake ni Watanzania wote na tumeona namna ambavyo Wizara ya Afya imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba bima ya afya inakuwa jambo la msingi kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na jibu la msingi la Serikali, Serikali inao wajibu wa kuwekeza kwenye michezo yote ndipo wafadhili wanafuatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, mchezo wa ngumi kama navyoutetea hauna ufadhili wa Serikali ili kupata timu nzuri itakayotuwakilisha kimataifa. Ni lini Serikali itaandaa maeneo ya wanamichezo hawa kufanya mazoezi ili waweze kuwa vizuri na kuweza kushinda katika timu za kimataifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Wizara husika, hasa kwenye ngumi, ameonesha jitihada za kusaidia wachezaji wa ngumi kwa sasa. Serikali kwa wachezaji wa ngumi wanaume tayari wameonesha jitihada ni lini sasa watafanya hivyo kwa wachezaji wa ngumi wa kike ambao bado wako nyuma kwenye vifaa vya kufanya mazoezi ili waweze kushinda? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu ni miongoni mwa mapromota wanawake wachache kabisa ambao tunao nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikianza na swali lake la kwanza ambapo amesema kwamba Serikali ina wajibu wa kuwekeza katika michezo yote. Ni kweli kwamba sisi kama Serikali tuna wajibu wa kusimamia lakini kazi kubwa ya Serikali ni kuandaa miundombinu na kuweka mazingira wezeshi ya kisera pamoja na sheria. Suala la ufadhili wa michezo yote nchini Tanzania ni la vyama pamoja na mashirikisho ambayo ndiyo yanasimamia michezo hiyo vilevile kwa kushirikiana na wadau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, sisi kama Serikali tunao mpango wa kuhakikisha kwamba tunafanya uwekezaji mkubwa zaidi katika michezo. Ndiyo maana umeona katika kipindi cha hivi karibuni nchi yetu imepata fursa ya kuweza kushiriki kwenye mashindano mbalimbali na sisi kama Serikali tumejipanga kuhakikisha kwamba tunaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha kwamba tunafanya ufadhili katika michezo mbalimbali ukiwepo mchezo wa ngumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye swali lake la pili pia ametaka kujua ni lini sasa Serikali itaanza kuweka mkakati kuhakikisha kwamba tunakuza mchezo huu wa ngumi. Kama ambavyo amezungumza ni kweli sisi kama Wizara ya Michezo kwa kipindi cha hivi karibuni tumefanya jitihada kubwa sana ya kuhakikisha kwanza tunaboresha mchezo huu wa ngumi na jambo la msingi ambalo tumelifanya ni kuhakikisha kwamba tunaunda Kamisheni ya mchezo huu wa ngumi. Lengo ilikuwa ni kuhakikisha kwamba mchezo huu wa ngumi unapata mafanikio makubwa kitaifa na kama ambavyo tumeshuhudia kwamba ni mchezo ambao tunaamini kabisa kama uwekezaji ukifanyika vizuri utakuwa na mafanikio makubwa

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi kwa upande wa Serikali tayari tulishaanza kuweka mikakati na matunda yameanza kuonekana ndiyo maana jana tulishuhudia wanamasumbwi watatu wamekuja hapa na mikanda ya kutosha kabisa. Kwa hiyo, kama Serikali tunatambua umuhimu wa mchezo huu na tunaahidi kwamba tutaendelea kufanya uwekezaji mkubwa vilevile kwa kushirikiana na wadau. Ahsante.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 12 (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatamka kwamba kila mtu anastahiki heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na matukio ya vyombo vya habari kuwadhalilisha na kuwasingizia uongo baadhi ya watu na katika watu wanaosingiziwa wengine wana uwezo wa kwenda Mahakamani na wengine ni wanyonge ambao hawana uwezo wa kusimamia hizi kesi Mahakamani. Je, Serikali inatoa msaada gani wa kisheria kwa watu ambao wanadhalilika na kukosa haki za utu wao kutokana na kusingiziwa na makosa kama hayo na vyombo vya habari? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, mara kadhaa nimeshuhudia baadhi ya magazeti kama Mwanahalisi na Tanzania Daima yakipewa adhabu mara kwa mara ya kufungiwa kutokana na kuzua au kuonekana wamesema uongo, lakini sijawahi kuona magazeti ya Tanzanite, Jamvi la Habari na Fahari Yetu yakichukuliwa hatua yoyote wakati ni kinara wa kuzua na kudhalilisha watu katika nchi yetu: Kwa nini Serikali haichukui hatua kwa vyombo hivi vya habari na mmiliki wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kutoa ufafanuzi kwa maswali ambayo ameuliza Mheshimiwa Mbunge. Kwanza niseme kwamba kitu ambacho anazungumza siyo kweli kwa sababu sisi kama Serikali tunafanya kazi kwa kusimamia sheria pamoja na kanuni. Mara zote ndani ya hili Bunge tumekuwa tukitoa ufafanuzi kwamba sisi kama Wizara tumekuwa tukichukua hatua kwa magazeti yote ambayo yanakiuka sheria ambazo sisi wenyewe Wabunge tumezitunga ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikirudi kwenye swali la Mheshimiwa Mbunge ambapo amesema kwamba hatuchukulii hatua magazeti ya Tanzanite, siyo kweli kwa sababu tumeshajibu mara kadhaa humu ndani kwamba tumeshaandikia onyo gazeti la Tanzanite, vilevile hata gazeti la Tanzania Daima pamoja na
kwamba mara nyingi limekuwa likikiuka hizo kanuni, lakini tumekuwa tukiliandikia onyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Sheria yetu ya Habari inazungumza kwamba kabla ya kuchukua hatua yoyote kwa chombo chochote cha habari, cha kwanza tunachokifanya, tunatoa onyo mara ya kwanza, tunatoa nafasi ya mara ya pili na pale ambapo tunaona sasa hali hiyo imezidi, ndipo ambapo tumekuwa tukichukua hatua ya kuweza kufungia hayo magazeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo kweli kwamba tumekuwa tuna upendeleo. Sheria haina upendeleo, nasi kama Wizara tumekuwa tukichukua hatua pale ambapo tunaona tumeshaonya mara kadhaa lakini bado hawajajirekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

NAIBU WAZIRI YA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida wananchi ambao wamekuwa hawana uwezo wa kifedha wa kupata huduma ya kisheria, wamekuwa wakisaidiwa kupewa huduma hiyo na Serikali kupitia Wanasheria wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, pale ambapo kuna changamoto yoyote ambayo inahusu malalamiko ya kutotendewa haki katika eneo lolote linalohusu sheria, basi mamlaka ya Serikali kupitia Wizara ya Sheria na Katiba wamekuwa wakichukua hatua ya kuwasaidia, kuwasikiliza na kuwashauri wananchi ambao wamekuwa wakihitaji huduma hizo za kisheria kwa ajili ya kuweza kufanikisha mashauri yao ama kesi zao mbalimbali aidha iwe Mahakamani ama kesi za kawaida za upatanishi na usuluhishi. (Makofi)
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa sasa lugha ya alama inatumika kwenye chombo kimoja tu cha TBC lakini TV stations zingine hazina ikiwa ni pamoja na TV station ya hapa Bungeni. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba TV stations karibu zote zina wakalimani na watafsiri wa lugha ya alama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipongeze pia maswali ambayo yamejibiwa na Naibu Waziri lakini kama ambavyo swali limeulizwa kwamba sisi kama Serikali tuna mpango gani katika kuhakikisha kwamba vyombo vyote vinatoa huduma ya ukalimani kwa watu ambao wana tatizo la ulemavu, sisi kama Serikali ambao tumekuwa tukisimamia masuala mazima ya habari, kwa upande wa TBC ni wazi kwamba tumeboresha na sasa hivi tuna wakalimani zaidi ya wanne na vipengele vyote muhimu ikiwepo taarifa ya habari na vipindi maalum, wakalimani wa lugha za alama wamekuwa wakitoa hizo tafsiri. Ni takwa la kisheria kuwa na wakalimani na sisi kama Wizara ambayo tunasimamia masuala ya habari tumekuwa tukisisitiza kwamba vyombo vyote vya habari vikiwepo vyombo vya umma pamoja na binafsi vihakikishe kwamba vinakuwa na wakalimani wa lugha za alama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kutoa wito kwa wamiliki wote wa vyombo vya habari kuhakikisha kwamba wanatekeleza takwa hilo la kisheria kwa kuwa na wakalimani wa lugha za alama. Nashukuru. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili y nyongeza, swali la kwanza natambua juhudi za Serikali zinazofanywa kuitangaza Kiswahili ili kiweze kutumika duniani mpaka kufikia kwamba Kiswahili sasa ni lugha rasmi inayotumiwa SADC, hatua hizo zinazofanya Serikali ni nzuri lakini ninalo swali moja.

Je, kwa kipindi hiki TBC kama TBC ina mkakati gani wa kuwa na translate kwenye vipindi vyake anaye translate Kiswahili kwenda kingereza, na kingerez akwenda Kiswahili wakati anatangaza taarifa zake za habari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni ukweli usiopingika kwamba kuna television na redio za TBC. Je, TBC kama TBC ina mkakati gani wa kukuza lugha hii duniani kwa kuongeza masafa yake nikiwa na maana frequency ziweze kusikika kwenye nchin mbalimbali duniani?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza kwa maswali mazuri ya nyongeza, lakini nikianza na swali lake la kwanza ametaka kujua kwamba TBC tuna mkakati gani kwa kuwa na mtafusiri kutoka kwenye lugha ya Kiswahili kwenda kwenye lugha ya kingereza. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu kangu la msingi kwamba kwa sasa hivi tunavyo vipindi mbalimbali ambavyo vinatangazwa kwa lugha. Kwa hiyo, naamini kwamba kupitia hivyo vipindi watu wa mataifa mengine kwa maana ya nchi za nje wanaweza kupata kila kitu ambacho kinaendelea ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija pia kwenye swali lake la pili anataka kujua kwamba tuna mkakati gani wa kukuza lugha ya ksiwahili duniani. Mimi niseme kwamba Mheshimiwa Taska Mbogo anatambua namna gani ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa mstari wa mbele katika kukuza Kiswahili, vilevile tunamshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu ndiye ambaye amewezesha sasa hivi kiswahili kinatumika kwenye mikutano ya SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme kwamba sisi kama Shirika la Utangazaji la Taifa mkakati wetu kuhakikisha ya kwamba tunakuza kiswahili na ndiyo maana tumekipa kiswahili kipaumbele katika vipindi vyetu, vilevile tumetengeneza apps mbalimbali ambazo zinapatikana ndani pamoja na nje ya nchi. Kwa hiyo, vipindi vyote ambavyo vinatangazwa ndani ya Tanzania, vilevile kwa kupitia app mbalimbali kwa maana ya mtandao wanapata taarifa mbalimbali ambazo zinatokea katika nchi yetu ya Tanzania, ahsante.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza naomba nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri na kazi nzuri ambayo inafanyika na Wizara hii. Pamoja na pongezi hizo naomba niulize swali la nyongeza, yako maeneo mpaka hivi tunavyozungumza yana tatizo la usikivu kwa upande wa TBC, yakiwemo maeneo ya Nyasa kule mipakani, baadhi ya maeneo katika halmashauri ya Wilaya ya Tunduru na hasa yale ya mipakani, badala ya kuwa na usikivu mzuri wa TBC sasa wanasikiliza redio za nje kama kule Nyasa.

Je, Serikali ina mkakati gani kupitia Wizara kuhakikisha maeneo yote sasa yanakuwa na usikivu mzuri ili wananchi waweze kuitumia fursa hii kupitia Shirika la TBC, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa maswali yake mazuri ya nyongeza, lakini kama ambavyo amezungumza sisi kama wizara tunatambua ni kweli kwamba tatizo la usikivu kwa baadhi imekuwa ni changamoto. Lakini Mheshimiwa Mbunge atakubaliana na mimi kwamba kwa kipindi cha hii miaka minne ya utekelezaji wa Serikali ya Awamu ya Tano kazi kubwa sana imefanyika katika kuhakikisha kwamba tunaboresha masuala ya usikivu wa TBC katika nchi nzima ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi tumeweza kufikia Wilaya 102, lakini wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani tulikuwa tuna Wilaya 52 tu ambazo zilikuwa zinapata usikivu wa TBC. Lakini malengo ambayo tunayo kwa mwaka huu 2019/2020 kwa bajeti ambayo tayari tumeshaipitisha ni kuhakikisha ya kwamba tunaongeza Wilaya 15 kwa maana utoke Wilaya 102 tuweze kuwa na usikivu katika Wilaya 117.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie fursa hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge pamoja na watanzania nzima kwamba sisi kama Serikali tumejipanga katika kuhakikisha kwamba tatizo la usikivu wa TBC katika nchi nzima ya Tanzania linaboreshwa na niwahakikishie kwamba kwa sasa hivi TBC iko vizuri na tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa sababu imekuwa ikiongeza bajeti kila mwaka lakini lengo kuhakikisha ya kwamba tunaboresha usikivu TBC, ahsante.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza. TBC imekuwa ikisikika kwenye baadhi ya maeneo ya nchi hii lakini katika Jimbo la Ludewa TBC haisikiki kabisa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba Jimbo la Ludewa na maeneo yake TBC inasikika?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Deogratias Ngalawa naomba niongezee kidogo. Ni kwamba juzi TBC imerusha Mkutano Mkuu wa Chama cha NCCR-Mageuzi. Kwa hiyo, kusema kwamba TBC ina ubaguzi siyo kweli. Tumekuwa tunafanya kazi na vyama vyote na TBC ni chombo cha Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye jibu la Mheshimiwa Deogratias Ngalawa, ametaka kujua ni lini sasa tatizo la usikivu wa TBC litaboreshwa kwenye Wilaya yake ya Ludewa? Niseme kwamba kwa sasa hivi kwenye mipango yetu ya bajeti ya mwaka 2019/2020 tumejipanga kuboresha mikoa mbalimbali ikiwepo Mkoa wa Njombe, Songwe, Simiyu pamoja na mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie fursa hii kuweza kumhakikishia Mheshimiwa Deogratias Ngalawa kwamba tatizo la usikivu wa TBC kwenye Wilaya yake na vilevile Mkoa mzima wa Njombe litaboreshwa muda siyo mrefu. Ahsante sana.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, sote tunatambua kuwa Redio Tanzania inaendeshwa na kodi za Watanzania na kwa sasa ni zaidi ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Redio Tanzania lakini maeneo ya pembezoni haisikiki na watu wanalazimika kusikiliza redio za nchi jirani. Hivi tunakwama wapi? Ni kwa nini TCRA isiondoe vikwazo kwa redio binafsi ili zipewe jukumu la kuhakikisha zinatoa huduma na kuwafikia Watanzania katika maeneo yote nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa nashukuru, hizi zote ni neema za Mwenyezi Mungu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Devotha Minja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nitumie fursa hii kumtoa hofu kwamba TCRA kwa maana ya Serikali haijaweka vikwazo kwa redio yoyote ya binafsi kuanzisha vituo vyake vya redio. Mara zote sisi kama Wizara ambao tunasimamia masuala yote ya habari lakini kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Mawasiliano, tumekuwa tukisisitiza kwamba milango iko wazi kwa mtu na taasisi yoyote ambayo inataka kuanzisha redio waweze tu kufuata zile taratibu ambazo zinatakiwa katika kuanzisha redio hizo.

Mheshimiwa Spika, vilevile, sisi kama Wizara ambao tunasimamia masuala ya habari nchini Tanzania tumekuwa tukihakikisha kwamba maeneo yote ya mipakani yanafikiwa na usikivu wa Redio yetu ya Tanzania. Katika kuthibitisha hilo, kwenye jibu langu la msingi nimesema wazi kwamba katika bajeti ya mwaka 2016/2017, TBC ilifanya uwekezaji mkubwa sana katika maeneo yote ya pambezoni ikiwemo katika wilaya zote ambazo zipo mipakani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Serikali tunatambua concern yake kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuboresha usikivu wa TBC pamoja na Redio Tanzania katika maeneo yote ya mpakani.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu hii ya Twiga Stars ni timu ambayo imeweza kushinda michezo mingi nje ya nchi na ni timu ambayo kwa kweli ina makombe mengi kushinda hata makombe mengine ambayo yapo ya timu zingine za wanaume zilizopo hapa Tanzania. Sasa Serikali haioni haja sasa ya kuwatambua, kuwathamini na kuwekeza katika timu hii ya wanawake ili hawa wanawake waweze kupata ajira ndani na nje ya nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, michezo ni ajira na soka hili la wanawake limekuwa ni ajira sasa hivi. Tunaona watoto wengi wa kike wamependa michezo. Kule Kalenga sasa hivi nikienda badala ya watoto wa kiume kuomba mipira ni wasichana wanaomba mipira kwa ajili ya kucheza soka la wanawake na tunaona nchi za Ujerumani, Japan na West Africa nchi zao zimewekeza na timu za wanawake zimeweza kushinda katika soka kombe la dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa je, Serikali ina mkakati gani wa muda mrefu wa kujenga academy za soka la wanawake hata kwa kila kanda ili kuwawezesha hawa wanawake wakajengewa vipaji na kwa sababu michezo ni ajira. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mazuri lakini nikianza na swali lake la kwanza ambalo ametaka kujua kwamba mpango wa Serikali ni nini katika kuwekeza kwenye Timu ya Twiga Stars?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba ni kweli Timu ya Twiga Stars imekuwa ikifanya vizuri sana kwa miaka mingi na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge umesema, kufanya vizuri kwa Timu ya Twiga Stars maana yake Serikali imefanya uwekezaji mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nikuhakikishie kwamba kama ambavyo tumekuwa tukifanya uwekezaji katika Timu ya Twiga Stars, tunaahidi kwamba tutaendelea kufanya uwekezaji zaidi ili timu hii ifanye vizuri lakini si Timu ya Twiga Stars peke yake ni pamoja na timu nyingine kwa sababu tunazo timu nyingi sana ambazo zinafanya vizuri na ni timu za wanawake ikiwemo timu ya Kilimanjaro Queens inafanya vizuri lakini pia tunayo timu nyingine ya Mlandizi Queens pamoja na timu zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uwekezaji ni mpango ambao kama Serikali tunao na tunaendelea kuufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lako la pili ambalo umetaka kujua kwamba Serikali tuna mpango gani katika kujenga academy. Nikuhakikishie kwamba sisi kama Serikali tumekuwa tukihamasisha sana kwa sababu tunatambua kwamba hatuwezi kuwa na timu kubwa za kitaifa kama hatujawekeza kwenye kujenga academy ambazo zitalea vijana. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tumekuwa tukitoa hamasa kwanza kwa wadau kwa mashirikisho lakini vilevile hata kwa Waheshimiwa Wabunge tuweze kushirikiana katika kuhakikisha kwamba tunajenga academy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie fursa hii kuwapongeza wadau wote ambao wameshirikiana na Serikali lakini wameunga mkono jitihada za Serikali katika kujenga academy ikiwepo academy ya kule Kaitaba lakini tunayo academy ya pale Filbert Bayi pamoja na wadau wengine ambao wanafanya kazi vizuri katika kuhakikisha kwamba tunawekeza katika kuwakuza vijana wetu ili siku moja tuweze kuja kuwa na timu ambazo ni bora zaidi. (Makofi)
MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba ruhusa yako kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza, niwapongeze Simba Sports Club kwa kuchukua ubingwa wa Tanzania mara mbili mfululizo. (Makofi)

MHE. ALLY SALEH ALLY: Mnajuana eeh! (Makofi)

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, mimi nina wasiwasi kwamba agizo analolitoa Mheshimiwa Waziri kwamba linafanyiwa kazi na vilabu na hili tatizo ni kubwa linajitokeza mara kwa mara: Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kuleta sheria hapa Bungeni kuvibana vilabu angalau vile vya daraja la kwanza na vile vinavyocheza Club Bingwa ya Tanzania kupima kwa lazima? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali langu ya pili, hili suala la upimaji wa afya, basi Bunge tungekuwa mfano mzuri sana, kwa sababu tuna vilabu mbalimbali vya michezo hapa Bungeni, mfano Club ya Mpira wa Miguu Ndugai Boys na michezo hii inashirikisha Viongozi Mashuhuri. Mfano mzuri Waziri Mkuu amekuwa mchezaji, pia amekuwa Kocha ambaye ameleta ufanisi mkubwa katika timu ya Bunge hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kujua, ni lini wamewahi kupima afya zao wakicheza michezo ya ndani? Au ile wanayotushirikisha katika Mabunge ya East Africa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri. Nikianza na swali lake la kwanza ambalo amezungumzia kwamba agizo hili huwa halifanyiwi kazi.

Mheshimiwa Spika, napenda nitumie nafasi hii kusema kwamba suala la kupima afya kwa wachezaji ni agizo ambalo sisi kama Wizara tunalisimamia. Ukiacha kwamba ni suala la kisera, ukiangalia kwenye kanuni za FIFA, vilevile kwenye kanuni za TFF imeelekeza wazi kwamba vilabu vyote na mashiriko yote ya mpira wa miguu yahakikishe kwamba yanapima afya ya wachezaji wao, siyo tu kipindi ambacho vilabu vinajiandaa kuingia kwenye mashindano, vilevile kabla ya usajili wowote kuweza kufanyika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo ni agizo, nasi kama Wizara tunalisimamia, lakini kwa ushauri ambao Mheshimiwa Mbunge ameutoa, kwamba sisi kama Wizara tulete sheria hapa Bungeni, niseme kwamba ushauri huo tumeupokea kwa sababu sisi Wabunge ndiyo ambao tunatunga sheria; na kama Mbunge ameona kwamba kuna haja ya kuwa na hiyo sheria, basi sisi kama Wizara tutakaa na kuangalia namna gani ambavyo tutaleta hiyo sheria ndani ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili amezungumzia kuhusiana na timu ya Wabunge. Ni kweli kwamba tunayo timu ya Wabunge na timu yetu imekuwa ikifanya vizuri sana katika mashindano mbalimbali ya East Africa. Kwa hiyo, kama ambavyo nimezungumza, suala la kupima afya kwa wachezaji siyo tu kwa timu ambazo zinashiriki ligi kuu, ni jukumu la timu zote ambazo zinashiriki mashindano mbalimbali, iwe ni timu ambazo zinashiriki ligi daraja la kwanza, daraja la pili, vilevile hata kwenye michezo ya UMISETA na UMITASHUMTA wanatakiwa kupima afya kwa wachezaji wao kabla ya kuanza kwa mashindano.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata kwa sisi Wabunge, ni jukumu letu la kuhakikisha kwamba wanapima afya zao kabla ya kuweza kushiriki mashindano yoyote au kabla ya kwenda kushiriki kwenye mashindano ambayo huwa yanafanyika nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika mchezo wa ngumi, asilimia 99 ya wachezaji wanapata maumivu. Je, ni lini Serikali italazimisha ma- promoter kuwakatia bima hasa mabondoa wanawake hapa nchini Tanzania? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza kwa sababu Mheshimiwa Sophia Mwakagenda ni promoter pekee mwanamke ambaye anashiriki kwenye michezo ya ngumi. Nikija kwenye swali lake la msingi ambalo ametaka kujua kwamba ni lini sasa Serikali tutasimamia hawa wanaocheza michezo ya ngumi kuweza kukatiwa bima; nikiri kwamba imekuwa ni changamoto ya muda mrefu kwamba wachezaji wengi ambao wanacheza michezo ya ngumi wamekuwa wakifanya kazi kwenye mazingira magumu ikiwepo kutokuwa na Bima za Afya.

Mheshimiwa Spika, kwenye hivi vyama ambavyo vinashiriki mchezo huu ndondi kumekuwa kuna migogoro ya muda mrefu sana na ndiyo maana wachezaji hawa wakawa hawapati ile haki yao ya kuweza kupata Bima ya Afya. Kwa sasa hivi kama Wizara, tumeshaunda shirikisho la kuweza kusimamia mchezo huu wa ngumi nchini Tanzania. Lengo mojawapo kwenye vile vipengele ambavyo tumeviweka, ni kuhakikisha kwamba ni lazima kwa Ma- promoter kuwakatia Bima za Afya wachezaji wao.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. JUMA KOMBO HAMAD:Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nina maswali mawili madogo sana ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kusema kwamba Serikali imeshindwa kuwapatia watanzania Vazi la Taifa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali namba mbili, nilitaka kujua tu, Serikali katika mchakato huu ambao kwa mujibu wa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema ulianza mwaka 2011, ni muda mrefu kidogo na ni mchakato ambao ulichukua muda. Anaweza kutueleza ni fedha kiasi gani za Watanzania ambazo zilitumika katika mchakato huo ambao hadi sasa haukukamilika na ile ndoto ya Watanzania kuwapatia vazi la taifa sasa imepotea? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza amezungumza kwamba Serikali imeshindwa kukamilisha mchakato wa kupata Vazi la Taifa. Napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali haijashindwa na Serikali haijawahi kushindwa na jambo lolote, hususan Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, kitu ambacho tunakifanya, kama ambavyo nimejibu yangu ya msingi kwamba kwa sasa hivi tumeshaufufua upya huo mchakato na nikuhakikishie kwamba Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato huo, muda si mrefu utaenda kukamilika.

Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuweza kutoa wito kwa Maafisa Utamaduni wote wa Mikoa yote ya Tanzania, lakini vilevile kwa Makatibu Tawala wote wa Mikoa ambao ndiyo tumewakabidhi hilo jukumu, ili Vazi la Taifa liweze kupatikana kuhakikisha kwamba wanasimamia huo mchakato uweze kukamilika kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikija kwenye swali lake la pili, kwa sababu ametaka kujua kuhusiana na fedha ambazo zimetumika kuanzia mchakato ulipoanza mwaka 2011. Niseme kwamba kwa sababu ni suala la kitakwimu, naomba baada ya hapa Mheshimiwa Mbunge tuweze kuonana ili niweze kukupatia hiyo takwimu. Ahsante.
MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika,kwa kuwa Watanzania wanapokwenda nje ya nchi sasa hivi wanatumia scarf, t-shirt za bendera za Taifa na tai kama hizi, ile Mwigulu style na wanatambuliwa kuwa ni Watanzania.

Kwa nini Serikali isiidhinishe tu kwamba scarf, tai za Taifa na bendera za Taifa ndiyo itakuwa vazi la taifa kwa sababu nchi hii hawawezi wakavaa uniform ili kutambulisha kwamba lile ndiyo Vazi la Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu yeye amekuwa mzalendo kwelikweli katika kuhamasisha masuala ya utamaduni nchini Tanzania, lakini vilevile kama amabvyo ametaka kujua kwamba vazi ambalo amekuwa akilitumia yeye binafsi mara nyingi, kwa maana ya vazi la tai ambayo ina bendera ya Taifa, kwanini sisi kama Wizara tusilirasimishe rasmi liweze kuwa Vazi la Taifa.

Niseme kwamba kwa sababu kwa sasa hivi kuna mchakato ambao tumeshauanzisha na tumeshaufufua ambao ni mchakato mpya, lakini pia niseme kwamba maoni ambayo ameyatoa tunayachukua na tutayafanyia kazi ili tuangalie kama kuna huo uwezekano. Ahsante sana.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu Mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya Nyongeza. Kwa kuwa Mfalme wa Morocco alikubali kujenga Uwanja wa Michezo wa Kimataifa hapa Dodoma:

Je, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko tayari kuwasiliana na Serikali ya Morocco ili ujenzi uanze mapema iwezekavyo?

Kwa kuwa Dodoma ndiyo Makao Makuu: Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga viwanja vingine vya michezo ili ikiwezekana Tanzania ije ipate nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa Michezo ya Kimataifa.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika swali la msingi, mawasiliano baina ya Serikali mbili za Tanzania na ile ya Morocco yanaendelea na ni tumaini letu kwamba muafaka utafikiwa mapema iwezekanavyo kuhusu mradi huu wa ujenzi wa uwanja wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa bado mpango wa kujenga uwanja mpya wa Dodoma unaendelea, Mheshimiwa Mbunge avute subira kwa sasa Serikali ikamilishe kwanza mradi huo na kisha Serikali itaweza kufikiria kujenga viwanja vingine zaidi na siyo lazima iwe Dodoma pekee, bali hata miji mingine inayozunguka Makao Makuu ya nchi itafikiriwa.