Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Josephine Johnson Genzabuke (37 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama ndani ya Bunge hili Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, kwa vile ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili la Kumi na Moja, napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa moyo wangu wa dhati kabisa wanawake wa Mkoa wa Kigoma kwa kunirejesha Bungeni kwa mara nyingine na mimi nasema sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa ushindi mnono alioupata. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wengine kwa kuteuliwa ku wa Mawaziri katika Baraza la Mawaziri la mwaka 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuendelea kuishukuru Serikali kwa moyo wangu wa dhati kwa kuendelea kufanya mambo mazuri katika Mkoa wa Kigoma. Naishukuru sana na naendelea kuwapongeza viongozi wa Awamu ya Nne walioweza kuufungua Mkoa wa Kigoma. Daima tutamkumbuka Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuweza kuufungua Mkoa wa Kigoma, lakini na aliyekuwa Waziri wa Ujenzi ambaye kwa sasa ni Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa waliyoifanya ndani ya Mkoa wa Kigoma. Walitujengea barabara, wakatujengea Daraja la Mto Malagarasi maarufu kwa jina la Kikwete, daraja kubwa ambalo ni mfano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi cha mwaka 2015 niliwahi kusimama nikasema wananchi wameona na kwa vile wameona hawatatuangusha. Wakati ule tulikuwa tukiitwa sisi ni wapinzani lakini tuliufuta upinzani sisi ni Chama Tawala. Naomba nimshukuru Katibu Mkuu na aliyekuwa Katibu Mwenezi kwa kazi kubwa waliyofanya ya kuwaelimisha wananchi wa Mkoa wa Kigoma Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilivyokuwa ikitekelezeka na hatimaye tukaweza kurejesha Majimbo yaliyokuwa yamepotea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa barabara zile ambazo hazikukamilika ikiwepo barabara ya Kigoma – Kasulu – Nyakanazi iweze kujengwa. Pesa zilizotengwa zipelekwe ili barabara ile iweze kukamilika. Pia kipo kipande cha kutoka Uvinza - Malagarasi kilometa 48 kwenda kwenye Daraja la Mto Malagarasi kwenye Daraja la Kikwete, naomba kilometa hizo ziweze kujengwa kusudi wananchi waweze kupata manufaa kupitia barabara hiyo. Kipo kipande kingine kutoka Chagu - Usinge - Kaliua, nacho naomba kiweze kukamilishwa kutuunganisha na Mkoa wa Tabora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 43 kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, amezungumzia kuhusu reli. Reli katika Mkoa wa Kigoma, Tabora na Ukanda wa Ziwa ni kilio kikubwa sana. Kabla reli nyingine haijajengwa tunaomba reli ya kati iweze kujengwa kwa sababu itakuwa ni mkombozi kwa wananchi wa Mkoa wa Kigoma, Tabora na Kanda ya Ziwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi huu wa reli tunaomba uwe ni wa kutekelezeka isiwe ni ahadi isiyotekelezeka kwa sababu kwa muda mrefu tumekuwa tukisema kwamba reli itajengwa, lakini haijengwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa wakati huu iwe ahadi ya kutekelezeka, isiwe ni ahadi isiyotekelezeka kwa sababu reli inaboresha uchumi. Reli ikijengwa wananchi wa Mkoa wa Kigoma pamoja na Tabora wataweza kunufaika na uchumi wao utaweza kuimarika. Reli itaweza kufungua fursa ya kibiashara kati ya nchi jirani na Kigoma itakuwa ni kitovu cha biashara. Watu wa Burundi, DRC wataweza kusafirisha mizigo yao kwa kupitia Mkoa wa Kigoma na reli hiyo ya kati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa muda mrefu kabisa wananchi wa Mkoa wa Kigoma mpaka sasa hivi barabara hazijaweza kukamilika vizuri na kwa sababu hiyo reli ndiyo usafiri wa bei nafuu. Kwa sababu sasa hivi mtu akitoka Kigoma kuja Dar es Salaam anatumia shilingi 70,000 hapo hajapata chakula njiani, kwa kutumia basi anaweza kufika Dar es Salaam kwa shilingi 100,000 lakini reli ikikamilika itawapunguzia gharama ya usafiri wananchi wataweza kusafiri kwa bei nafuu na wataweza kusafirisha mizigo yao kwa bei nafuu lakini gharama za maisha nazo zitashuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sasa hivi mfuko wa cement Dar es Salaam shilingi 13,000 mpaka shilingi 14,000, lakini Kigoma shilingi 19,500. Tunaomba reli ikamilike ili wananchi wanaotumia reli waweze kunufaika lakini hivyo hivyo kwa kupitia reli uchumi uweze kukua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kuzungumzia kuhusu elimu. Kwanza naomba niipongeze Serikali kwa kuondoa ada kwa wanafunzi. Watoto wengine wa shule walikuwa wanafichwa kwa sababu ya ada lakini kwa sababu ada imeondolewa wanafunzi sasa wamepelekwa shuleni kwa wingi. Darasa la kwanza mwaka huu tumeona wameanza kwa wingi na ninaamini wataendelea hivyo hivyo ni kwa sababu Serikali imeondoa ada kwa wanafunzi. Naomba ada hii isiwe tangu darasa la kwanza mpaka form four iendelee mpaka form six ili watoto waweze kusoma kwa wingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuondoa ada tuangalie sasa ni jinsi gani tunawekeza katika elimu. Ninaamini watoto watakaomaliza form four watakuwa wengi, wengine watabahatika kuendelea na wengine wengi hawataendelea watarudi kukaa vijijini. Kwa hiyo, naomba kabisa Serikali iwekeze katika kujenga vyuo vya VETA ili watoto wanaomaliza kidato cha nne na pengine form six waweze kwenda kusomea VETA, hatimaye wajiajiri katika shughuli za mikono. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba niwasemee walimu ambao wanadai stahiki zao nyingi. Wapo walimu ambao wamepandishwa madaraja na wamestaafu na walikiri kupanda daraja lakini mpaka wanastaafu mishahara yao haijaweza kurekebishwa. Nilitaka kuuliza, je, Serikali itafanya marekebisho kwa kutumia mishahara yao pale walipopanda madaraja? Kama si hivyo, naomba Waziri anayehusika wale ambao watakuwa na malalamiko wamepanda daraja mishahara haijarekebishwa waweze kurekebishiwa mishahara yao kusudi wanapotapa pesheni zao iendane na mishahara yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie maji. Maji ni afya, maji ni uhai. Kwa muda mrefu wanawake wa Tanzania wameendelea kuteseka kwa kukosa maji. Sisi Tanzania tumejaliwa kuwa vyanzo vingi vya maji, tumejaliwa kuwa na bahari, maziwa, mito mikubwa na modogo.
Kwa hiyo basi, naomba Serikali ijipange kutumia vyanzo hivyo ili kuweza kufikisha maji vijijini na kuwaondolea adha wanawake ambao wamekuwa wakipata shida kufuata maji kwa umbali mrefu na kukosa muda wa kufanya shughuli za kuwaletea maendeleo na kuinua kipato chao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Kasulu ipo miradi iliyoanzishwa lakini miradi hiyo haijaweza kukamilika kwa sababu fedha zimekuwa hazipelekwi. Naomba sasa katika bajeti hii fedha zipelekwe ili miradi iliyoanzishwa katika Wilaya ya Kasulu iweze kukamilika. Ipo miradi ya Kasangezi, Ahsante Nyerere, Helushingo na Nyarugusu.
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umemalizika.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuunga mkono hoja hii.
Kwa kuwa watu wanaongezeka lakini ardhi haiongezeki naomba Serikali ilete sheria Bungeni ifanyiwe marekebisho ili mipaka isogezwe ili kusudi wananchi wapate maeneo ya kulima. Mfano, katika Wilaya ya Kasulu lipo eneo la Kagera Nkanda eneo hili wananchi wanalima huko lakini mara nyingi wanaondolewa. Naomba Serikali iweze kumaliza tatizo hili la kuongeza mipaka ili wananchi wapate eneo la kulima. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri George Simbachawene na Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Waziri, Mheshimiwa Jafo pamoja na Viongozi wote walioko kwenye Wizara zao. Nawapongeza kwa hotuba zao nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu suala la afya, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa kutembelea hospitali ya Muhimbili, baada ya yeye kutembelea Muhimbili huduma zimeboreka, hakukuwa na kipimo cha MRI, MSD imeanzisha duka pale Muhimbili, wananchi wanapata huduma ya kupata dawa kwa bei rahisi. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie Mkoa wetu wa Kigoma. Serikali kwa kushirikiana na wananchi walijenga vituo vya afya, wakajenga zahanati, hii ni katika nchi nzima, lakini zahanati pamoja na vituo vya afya vilivyojengwa havina watumishi. Watumishi limekuwa ni tatizo, dawa limekuwa ni tatizo, vifaa tiba limekuwa ni tatizo. Kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Kigoma, Mkoa wa Kigoma una Wilaya saba, Mkoa wa Kigoma umekumbwa na wimbi kubwa la Wakimbizi. Wakimbizi wanatibiwa kambini lakini wakati mwingine wanaletwa kwenye hospitali za wilaya. Mkoa wa Kigoma hauna Daktari Bingwa, Hospitali ya Maweni Daktari Bingwa ni mmoja tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hebu fikiria, wananchi wa Wilaya zote saba wanapewa rufaa, wanapelekwa kwenye hospitali ya Maweni ambayo ndiyo hospitali ya Mkoa, lakini Daktari Bingwa ni mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuletewe Madaktari katika Mkoa wa Kigoma. Najua Muhimbili wapo Madaktari wa kutosha lakini huku Mikoa ya pembezoni Madaktari hawatoshi. Kwa kuuangalia Mkoa wa Kigoma naomba upewe kipaumbele kutokana na wimbi kubwa la Wakimbizi kutoka DRC na Burundi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Kasulu lipo vile vile tatizo la upungufu wa Watumishi, hatuna ultra sound, wanawake wanateseka, wanapata shida wanapokwenda kuambiwa wapimwe, wanakuta ultra sound hamna, hawawezi kujua mtoto amelalaje tumboni, kwa hiyo wanalazimika kwenda katika hospitali za kulipia. Naomba tuletewe ultra sound kuwaondolea adha wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Wauguzi ni wachache, utamkuta Muuguzi mmoja pengine yupo kwenye wodi ya akinamama, akinamama wanaotaka kujifungua wako nane ama kumi, Wauguzi wapo wawili, wanawake wanaohitaji kujifungua wako kumi, hebu angalia tofauti iliyopo, watu wawili kuhudumia watu kumi! Matokeo yake wanawake wanapoteza maisha na wakati mwingine watoto wanazaliwa wakiwa wamekufa? Naomba tuongezewe Waganga pamoja na Wahudumu wa Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuzungumzia suala la maji. Nimewahi kusema Tanzania tumejaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji; maziwa, mito mikubwa na midogo lakini maji yamekuwa ni tatizo kubwa linalowakumba wanawake. Naomba Serikali itenge pesa kwa ajili ya kufikisha maji vijijini ili kuwaondolea adha wanawake ambao wamekuwa wakiteseka kwa muda mrefu. Utamkuta mwanamke muda mwingi anatumia kwenda kutafuta maji, anashindwa kufanya shughuli za uzalishaji mali. Kwa hiyo, naomba Serikali itenge pesa, ipeleke pesa ili maji yaweze kufikishwa vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mji wa Kasulu lipo tatizo la mabomba kutoa maji machafu, Serikali imekuwa ikitenga pesa kupeleka Kasulu kwa ajili ya kuanzisha miradi iliyokwishaanzishwa katika Wilaya ya Kasulu. Naomba kupitia bajeti hii mtupelekee pesa ili miradi iliyoanzishwa iweze kukamilika. Mtupelekee pesa kwa ajili ya Mji wa Kasulu ambao maji yanatoka machafu bombani ili maji yaweze kutibiwa, kwa sababu maji yakiwa siyo salama ni hatari kwa maisha ya binadamu. Ipo miradi ya Kasangezi, Ahsante Nyerere, Heluwishingo na Nyarugusu pamoja na Nyumbigwa naomba pesa zipelekwe ili miradi hiyo iweze kukamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Walimu walipwe stahiki zao kwa sababu ni kilio cha muda mrefu. Walimu wanateseka sana wakati mwingine Mwalimu anahamishwa kutoka kituo hiki kupelekwa kituo kingine lakini halipwi pesa ya uhamisho. Siyo hivyo tu Walimu wanapata shida, hela za matibabu hawapewi, sisi tunapata pesa ya matibabu lakini Mwalimu hapewi pesa ya matibabu, hivi kwa nini Mwalimu anatengwa? Wakati mwingine anaweza kwenda akapewa hata sh. 20,000 au sh. 40,000. Hivi kweli mtu unampa sh. 20,000 au sh. 40,000, shika hizi kwanza zikusaidie halafu nyingine utadai! Naomba watendewe haki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wastaafu nao; naomba wanapostaafu pesa zao ziwafikie mara moja, wengine wamekuwa wakistaafu wakiwa wamerekebishiwa mishahara, lakini Serikali inashindwa kurekebisha mishahara yao kulingana na jinsi walivyopanda madaraja, matokeo yake wanastaafu wakiwa na mishahara ile ambayo walikuwa nayo huko nyuma. Ile ambayo wamepandishwa madaraja na wamekiri kupanda daraja inachelewa kufanyiwa marekebisho, matokeo yake wanapata pensheni ambayo hailingani na mishahara yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuja na wazo la kukarabati shule za sekondari ambazo ni kongwe, kwa mfano, Tabora Boys, Tabora Girls, Pugu na kadhalika. Naomba Serikali itenge pesa na Kigoma Sekondari nayo iweze kukarabatiwa, hii ni shule kongwe, naomba Serikali iweze kuikumbuka Sekondari ya Kigoma ambayo ndiyo amesoma Mheshimiwa Zitto, amesoma Kigwangallah, na wengine wengi. Naomba shule hiyo ikumbukwe, ni shule kongwe nayo ipelekewe pesa kwa ajili ya ukarabati.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo kuhusu milioni 50. Naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutenga shilingi milioni 50. Imekuwepo mikakati mingi kwa muda mrefu ya kutenga pesa kwa ajili ya kuwapelekea vijana na wanawake, lakini mipango hiyo imekuwa haitekelezeki, zilipelekwa pesa kidogo kidogo kupitia SIDO, kupitia SELF…..
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja hii ya hotuba ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu umeme wa REA Awamu ya Tatu, naomba Serikali inieleze ni lini mradi huo wa REA Awamu ya Tatu utafika Kigoma? Na ninaomba utakapofika Kigoma uweze kufika Kasulu hasa katika vijijji vyote vilivyopo katika barabara kuu
ya Kigoma - Nyakanazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, kwa kuanza kabisa, naunga mkono hoja hii.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Kigoma maeneo ya Wilaya ya Kibondo, hali ya usalama bado siyo nzuri. Hakuna utulivu pamoja na Serikali imejitahidi lakini bado matukio yapo ya mara kwa mara. Naomba Serikali ituwekee Mkoa Maalum wa Kipolisi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE.JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, namshukuru Mungu kwa kunijalia afya kwa mara nyingine kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Hasna Mwilima kwa kushinda kesi ya uchaguzi katika Jimbo la Uvinza. Kwa niaba ya wanawake wa mkoa wa Kigoma ninampongeza sana na ninamshukuru Mungu kwa kuweza kutenda maajabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana CCM tulikuwa tunaitwa wapinzani, lakini kwa utekelezaji mzuri wa Sera za CCM Mkoa wa Kigoma waliamua kuachana na upinzani wakarudi kukitendea haki Chama cha Mapinduzi. NCCR Mageuzi wakati ule walikuwa wanasema wao ndio Chama Tawala sasa Kigoma Chama cha NCCR Mageuzi kwisha kabisa, chali cha mende, nyang‟anyang‟a. Tumebaki na …
Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kuzungumza hayo…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Genzabuke, endelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti niliwahi kuwaambia, kwa mambo makubwa yaliyofanyika Kigoma..
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mambo yalifanyika Kigoma wananchi wa Kigoma waliamua wakasema, sasa NCCR basi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo za kumpongeza Hasna, naomba nianze kuchangia. Mkoa wa Kigoma tutaendelea kumkumbuka Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kuweza kuufungua mkoa wa Kigoma akiwa na Waziri wa Ujenzi ambaye ndiye Rais wetu, Mheshimiwa John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amefanya matendo makubwa sana, amejenga barabara za lami tunazopita, wana CCM na wapinzani wote ni mashahidi, zilijengwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanasema barabara zimeharibika. Kumbukeni mvua zikinyesha barabara zinaharibika, magari makubwa yakipita barabara zinaharibika, kwa hiyo ndugu zangu ambao mnasema Mheshimiwa Rais hajafanya chochote; mwaka jana wakati anawasilisha bajeti yake akiwa Waziri wa Ujenzi kwa kumbukumbu zangu nakumbuka kabisa Wabunge wote tuliipitisha bajeti ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kwa kura za ndiyo bila kupinga bajeti ile, wote tunaamini ni mchapakazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana mwaka wa jana tulipokwenda kwenye uchaguzi hatukuhangaika kumnadi Mheshimiwa John Pombe Magufuli, alijiuza mwenyewe kwa sababu ya utendaji wake uliotukuka.
Ninaomba kusema, kwa barabara ambazo tayari zimeshafunguka, naomba sasa barabara ya Kigoma – Nyakazi, Kigoma – Kasulu kilometa 50, Nyakanazi – Kibondo, kilometa 50, nashukuru kwa kutengewa pesa. Ninaomba sasa barabara ya kutoka Kibondo – Kasulu mpaka Manyovu nayo iweze kutengewa pesa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumekuwa tukisifika kwa kuwapokea wakimbizi, lakini watu wanaobeba mzigo mkubwa wa kuwapokea na kuwabeba wakimbizi ni watu wa Kigoma. Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Waziri ambaye mwaka huu kabla ya bajeti hii ulitoka Kibondo, Kasulu mpaka Kigoma ukaone kile kipande cha kilometa 258 ambacho ndicho kimebaki hakijatengewa pesa. Kipande kile ndicho kinachotumika kupitisha wakimbizi wanapotokea Burundi kupita Manyovu, kuja Kasulu kwenda mpaka Kibondo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kipande hicho kitengewe pesa mara moja ili na chenyewe kiweze kukamilika.
Ninaomba kipande cha kutoka Uvinza mpaka daraja la Kikwete kiweze kutengewa pesa ili kikamilike ikiwa ni pamoja na kipande cha Chagu mpaka Kazilambwa na chenyewe kiweze kujengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie kwenye reli. Huu ni mwaka wangu wa 11 nikiwa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muhuri ya Muungano wa Tanzani. Mimi kwa kushirikiana na Wabunge wa mkoa wa Kigoma, Shinyanga, Mwanza, Tabora, Mara, Rukwa Katavi na Kagera kilio chetu kikubwa kimekuwa ni reli. Tunaomba basi mipango ya ujenzi wa reli inayowekwa iwe ni ahadi inayotekelezeka, isije kuwa ni ahadi isiyotekelezeka. Ipangwe kujenga kwa standard gauge ili wananchi waweze kunufaika na matunda ya nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa mkoa wa Kigoma, na mikoa yote hiyo niliyoitaja wanapata shida sana kutokana na ukosefu wa usafiri wa uhakika wa reli. Akina mama wanapata shida, wanateseka, wanafunzi wanapokwenda shuleni wanapata shida sana. Tunaiomba Serikali, iweze kutekeleza ahadi ya kujenga reli ili kuwaondolea shida wananchi wanaoishi ukanda huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nimeangalia katika kitabu hiki sijaona kama imetengewa pesa kwaajili ya ukarabati wa bandari ya Kigoma. Ninaomba tunapokwenda kujenga reli na bandari ya Kigoma nayo itengewe pesa kwa ajili ya kutengenezwa. Kwa sababu mizigo ikisafiri kupitia reli ni lazima itafika bandarini, ikifika bandarini itasafirishwa kwenda DRC na Burundi. Kwa hiyo sambamba na kutengeneza reli tunaomba na bandari nayo iweze kuangaliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, meli ya Liemba ina miaka 100; meli ile ipo kabla ya uhuru, naomba iwekwe meli nyingine ya kusaidia meli ile. Tunapoteza mapato mengi sana kwa sababu meli tuliyonayo imechoka, imezeeka, kwa hiyo tunaomba tupatiwe meli nyingine. Lakini vilevile tunaweza hata tukapewa boti hizi za fiber boat kusudi ziweze kusaidia kusafirisha mizigo kutoka Kigoma kupeleka Burundi na DRC. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kiwanja cha ndege cha Kigoma. Ninaomba kiwanja hicho kiweze kutengewa pesa, kipanuliwe ili ndege ziweze kutua na kuruka. Ndege kubwa haziwezi kuruka kwa sababu uwanja ule maeneo ya kuruka ni kidogo. Naomba kipanuliwe ili ndege kubwa ziweze kuruka. Kwa sababu kiwanja kile kikiweza kutengenezwa kikawa na maeneo ya kuruka na kutua ndege kubwa watu wataweza kufanya biashara muda wote, tofauti na ilivyo sasa ndege ikienda asubuhi ikifika kule mchana hakuna ndege nyingine inayoweza kutua jioni au usiku.
Kwa hiyo, naomba kiwanja kile kiweze kutengenezwa. Lakini vile vile kule kwetu kuna hifadhi ya Gombe watalii wataweza kuja kwa wingi kutoka maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Chuo cha Hali ya Hewa Kigoma naomba kitengewe hela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika bajeti hii. Kwanza kabisa napenda kukupongeza kwa jinsi unavyoliendesha Bunge hili kwa umahiri na kwa weledi.

Naomba muda wangu ulindwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakupongeza kwa jinsi unavyoendesha Bunge kwa umahiri mkubwa na kuonesha uwezo wako ni jinsi gani unavyojua kuzitumia kanuni. Wembamba wa reli lakini inabebe mizigo mizito ni sawa na wewe. Hongera sana na sisi tunakwambia kazi buti, wanawake tupo nyuma yako, umethibitisha ni jinsi gani unavyoweza, wanawake wa Bunge hili na wanawake wa Tanzania tunakupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kaka yangu Philip Mpango, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa hotuba yao ambayo kwa kweli imesheheni mambo mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu sana nimekuwa nikisimama kuililia barabara ya Kigoma-Nyakanazi, huu mwaka wangu wa kumi na moja sasa, lakini siku hii ya leo nina furaha kubwa sana. Nafuraha kwa sababu nitakapoondoka ndani ya Bunge hili kuelekea Kigoma ninacho cha kuwaambia wananchi wa Kigoma maana najua kwa vyovyote wataniuliza ulizungumziaje barabara ya Kigoma-Nyakanazi, kwa hiyo nina majibu. Naomba sasa pesa zile zilizoelekezwa kwenda kujenga barabara ya Kigoma Nyakanazi zipelekwe ili barabara ile iweze kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kigoma ni kati ya mkoa ambao umeoneshwa kwamba ni mkoa maskini sana kati ya sababu zilizokuwa zinafanya tuwe maskini ni pamoja na miundombinu. Hata hivyo, kwa bajeti hii naomba niseme kwamba sasa umaskini tunauaga, kwa sababu wananchi watakuwa na miundombinu mizuri, watalima mazao yao, watasafirisha kwa kupitisha kwenye barabara nzuri, watasafirisha kupeleka mikoa mingine na kusafirisha ndani ya mkoa ule wa Kigoma; kwa hiyo naamini ule umaskini utaondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa Kigoma sisi ni wakulima wazuri sana, kwa hiyo naamini miundombinu ya barabara na reli ikikamilika umaskini utapungua, wananchi wataweza kupata maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie jeshi la zimamoto. Kwa muda mrefu sana tumeshuhudia wananchi wakipata hasara sana, maduka yanaungua, vitu vyao vinaungua, mitaji yao inapotea kwa sababu wanakuwa wamepata hasara kutokana na moto ambao unakuwa umeteketeza mali zao. Ni kwa sababu jeshi la zima moto halina vitendea kazi, tumeshuhudia sekta ya ujenzi inakua kwa kasi sana, tunashuhudia ujenzi wa majengo mbali mbali yakiwemo maghorofa yenye ghorofa tisa, kumi, ishirini mpaka thelathini na mbili, lakini jeshi la zima moto halina vitenda kazi, halina vifaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo wawekezaji wanaweza kuogopa kuja kuwekeza mali zao huku kwa sababu zimamoto hawana vifaa vya kuweza kutumika pale linapotokea janga la moto. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuliangalia hili. Katika bajeti hii inayotengwa sasa jeshi halijawezeshwa. Naomba hili nalo waliangalie jeshi la zimamoto litengewe fedha kwa kipindi kingine kama wakati huu haitawezekana kusudi wajiandae kukabiliana na majanga ya moto.
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi tu Nzega maduka yameteketea ni kwa sababu hakuna vifaa vya zima moto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka kuzungumzia kuhusu lishe. Serikali ilitoa agizo kwa Halmashauri zote kutenga bajeti shilingi tano tu kwa kila mtoto. Agizo hili lilitolewa ili kila mtoto atengewe Shilingi tano tu kwenye kila Halmashauri. Lakini mpaka sasa Halmashauri imepuuza maagizo hayo na sisi wote tunashuhudia watoto wetu wakati mwingine wakienda shule wanashindwa kufanya vizuri kwa sababu wanapokuwa shuleni wakati mwingine wanakuwa na njaa. Kwa hiyo, naomba Halmashauri zitekeleze agizo lililotolewa na Serikali la kutenga ile Shilingi tano kwa kila mtoto ili watoto wetu waweze kufanya vizuri. Maana nikiuliza ni Halmashauri ngapi ambazo zimetekeleza agizo hilo, jibu ni hakuna.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu bado ina tatizo kubwa la utapiamlo, Serikali imefanya jitihada kubwa sana kuweza kuweka virutubisho kwenye vyakula vinavyozalishwa viwandani, lakini wanaonufaika ni wenye viwanda, wazalishaji wale wakubwa wakubwa. Naomba sasa Serikali iwawezesha wajasiriamali wadogo wadogo ili na wao waweze kupata hivyo virutubisho waweze kuweka kwenye biashara zao zile ndogo ndogo ili na wao waweze kupata soko wasihangaike kwa kusumbuliwa kwamba vyakula vyao havina virutubisho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maji. Mkoa wa Kigoma nimeona tumetengewa pesa kwa ajili ya maji, naomba pesa hizo zipelekwe, lakini nashauri; Mkoa wa Mwanza kwa kupitia Ziwa Victoria waliweza kufikisha maji Shinyanga, Geita, wakafikisha maji Igunga na Tabora; naomba sasa na sisi Kigoma tuweze kutumia maji ya Ziwa Tanganyika. Uangaliwe utaratibu wa kuweza kufanya mipango ya kuweza kuyatumia maji ya Ziwa Tanganyika. Hii ni kwa sababu mito tuliyonayo sasa hivi inakauka, maji baadaye yatatoweka, lakini tukitumia Ziwa Tanganyika tutaweza kupata maji mengi kama wanavyopata maji kwa kupitia Ziwa Victoria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, milioni 50 zitakazopelekwa kwenye kila kijiji naomba Serikali ipange utaratibu mzuri. Mimi natokea huko vijijini, wanawake wamejipanga kuzisubiri shilingi milioni 50 lakini elimu hawajapata. Naomba elimu ipelekwe, watu wajiandae ni jinsi gani watapokea hizo pesa na kuziendeleza zisiwe kama pesa za JK, kwa sababu wengine watazipokea watafikiri ni zawadi wakati zinatakiwa pesa zile zikifika kule upangwe utaratibu ili ziweze kukopeshwa kwa watu wengine baadaye. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu afya. Wananchi kwa kushirikiana na Serikali walijenga vituo vya afya, wakajenga zahanati lakini…

Mheshimiwa Naibu Spika, hazijaweza kukamilika naomba Serikali ipeleke pesa ili vituo vya afya na zahanati ziweze kukamilika. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa rehema kwa kunijalia kusimama kwa mara nyingine ndani ya Bunge hili Tukufu. Haikuwa kazi rahisi lakini Mungu ni muweza wa mambo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru wana CCM wenzangu, lakini nikimshukuru Mwenyekiti wa chama changu na viongozi wakubwa wa chama kwa kuniombea. Mimi naomba niseme nitaendelea kuwa mwana CCM mwaminifu, muadilifu kwa kukipigania na kukitetea chama changu mpaka tone la mwisho la damu yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kuhusu kilimo. Asilimia kubwa ya Watanzania na hasa wanawake, wengi ni wakulima. Ukifanya sensa utawakuta wanawake wa Tanzania wanaongoza katika shughuli za kilimo. Kwa hiyo, ninachotaka kusema ni kwamba mvua za kwanza ni za kupandia. Ukichelewa kupeleka mbegu wakati mvua zinaanza kunyesha wananchi hawawezi kupata mazao mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengi wananchi walipanda bila pembejeo kwa sababu zilichelewa kwa maana ya mbegu, dawa na mbolea kwa ujumla. Hata wakati mwingine waliweza kupanda kwa kutumia mbegu ambazo ni tofauti na mbegu walizotegemea kupata, kwa hiyo, sehemu nyingine mazao yao hayakuweza kuwa mazuri. Naomba basi Serikali ijitahidi kuwahisha kupeleka pembejeo. Vilevile kutokana na ufinyu wa bajeti ya Wizara ya Kilimo, mwaka huu wananchi wengi hawakuweza kupata mbolea, walipata mbolea kiasi kidogo sana ambayo haikuweza kuwatosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hekima yake. Namshukuru sana kwa sababu leo hii ameweza kukutana na mawakala wa Tanzania walioweza kuwawakilisha wenzao akakaa na kuzungumza nao. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa usikivu wako. Kutokana na kazi ulizonazo isingeweza kuwa rahisi kuweza kuwakubalia kukaa nao, lakini umetumia nafasi yako kuweza kuwasikiliza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kutokana na jinsi ulivyowaahidi, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, watakapokuwa wamefanya utafiti, najua wako mawakala wengine sio waaminifu, tunafahamu wapo wengine ni waaminifu na wengine sio waaminifu. Kwa hiyo, wale ambao ni waaminifu watendewe haki na wale ambao sio waaminifu, wachakachuaji wasiwaponze wenzao, wale ambao watakutwa wamefanya vizuri, hawakuweza kuliibia taifa hili waweze kulipwa mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitumie nafasi hii Mheshimiwa Waziri Mkuu kueleza kwamba wananchi wengi walikopa wakati wanafanya kazi ya uwakala. Naomba muwasaidie kuwaombea kule kwenye mabenki wakati wanasubiri kulipwa haki zao mabenki yale yaweze kusitisha kuuza mali zao ili watakapopata pesa zao waweze kwenda kulipa mikopo yao. Mheshimiwa Waziri Mkuu, chonde chonde kupitia Waziri wa Fedha, tunaomba aongee na mameneja wa mabenki mbalimbali ambako wananchi walikopa mikopo, waweze kusubiri. Wananchi watakapokuwa wamelipwa madeni yao waweze kwenda kulipa madeni yale kwenye mabenki, watu wengi wanapoteza maisha kwa sababu mtu akiuziwa nyumba yake na hana njia nyingine, hana nyumba nyingine anapoteza maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu vituo vya afya na zahanati. Tuliahidi kujenga zahanati na vituo vya afya katika kila kijiji na kila kata. Kwa bahati mbaya yapo majengo ambayo tayari yalishajengwa hayajaweza kukamilika na ili yakamilike Halmashauri ndizo zinazotakiwa kujenga yale majengo na Halmashauri hazina pesa. Naomba Serikali isaidie Wizara ya Afya ili Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Halmashauri waweze kupeleka pesa kumalizia vituo vile vya afya na zahanati zilizoko kule kwenye vijiji na kata zetu ilia kina mama na watoto waendelee kupata huduma bora kutokana na vituo vitakapokuwa vimefunguliwa katika Wilaya zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza wanawake wa Tanzania. Wanawake wa Tanzania wameweza kuungana pamoja wakaanzisha vikundi mbalimbali, wakaanzisha vikundi vya SACCOS na SACAS. Naomba niseme vikundi vilivyo vingi havina elimu, vinaishia kukopeshana vyenyewe kwa vyenyewe kwa sababu havijaungana pamoja na hakuna sheria ambayo imeshaundwa kwa ajili ya kuvilinda vikundi hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba basi Serikali iweze kutunga sheria mahsusi ili vikundi hivyo viweze kuendeshwa kitaalam na viungane pamoja kusudi viweze kutambulika katika mabenki hatimaye viweze kukopesheka kwa sababu mabenki siyo rafiki wa maskini. Wale wenye vikundi
hawajaweza kwenda kufungua akaunti kwenye benki, wanakopeshana wao wenyewe huko mitaani kila baada ya mwaka wanafanya sherehe, wananunua nguo mpya, wanapika wali, wanavunja vikundi wanagawana na benki kama hawana sehemu ambayo wataenda kuangalia vikundi vinafanyaje hawawezi kukopesha wanawake hao na vikundi mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia kuhusu maliasili na utalii pamoja na Wizara ya Ardhi. Waliahidi kuunda Tume, Tume iliundwa kwenda kutembelea maeneo yenye migogoro, lakini kabla ya matokeo ya ile Tume iliyoundwa baadhi ya watu wamefukuzwa. Tunaomba basi
Serikali iweze kufanya haraka kutoa matokeo ili kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji na kuweza kusogeza mipaka baadhi ya maeneo ili wananchi waweze kupata maeneo ya kulima kwa sababu watu wanaongezeka, ardhi haiongezeki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuzungumzia maji kwa sababu mimi ni mama nafahamu adha wanayokutana nayo akina mama vijijini na hata mijini. Mwaka jana Mkoa wa Kigoma tulitengewa fedha za kutosha, lakini mpaka sasa hivi bado tuna tatizo la maji hasa Wilaya ya Kasulu ninayoishi mimi yako maeneo ambayo maji hayajaweza kufika. Katika eneo la Kibondo maji bado ni tatizo pamoja na Kakonko. Kwa hiyo, naomba zile pesa zilizotengwa, zisiondoshwe mahali pale ziweze kurudishwa Kigoma zikafanye kazi kuwaondolea adha wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho nataka kuzungumzia kuhusu barabara. Mara nyingi pesa za kutengeneza barabara zimekuwa zikipangwa lakini wakati mwingine hazipelekwi jinsi zilivyopangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba basi pesa zinazopangwa kwa ajili ya barabara za Kigoma ziende jinsi zilivyo ili tuweze kukamilisha barabara ambazo zimeshaanza kujengwa na hasa kipande cha kutoka Uvinza kwenda Malagarasi, Malagarasi kwenda mpaka Kaliua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami naomba niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia mambo matatu tu, la kwanza upungufu wa watumishi; pili, maboma ya zahanati pamoja na vituo vya afya ambayo yalijengwa kwa nguvu za wananchi pamoja na Serikali ambayo hayajakamilika, lakini la mwisho, itakuwa ni kuhusu maendeleo ya jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, mwaka wa jana Mheshimiwa Waziri alitembelea Mkoa wa Kigoma, alipitia karibu Wilaya zote na aliweza kujionea matatizo yaliyopo Kigoma. Mkoa wa Kigoma umekumbwa na wimbi kubwa la wakimbizi waliotoka Burundi, DRC kuja Kigoma, kwa hiyo watu ni wengi sana, wapo watu ambao wako makambini. Kama unavyojua binadamu huwezi kumzuia, wapo wakimbizi wengine ambao wamezagaa katika Wilaya zetu. Kwa maana hiyo basi, katika hospitali zetu watu ni wengi sana,


kwa hiyo tuna kila sababu ya kuongezewa Madaktari na Manesi ili kuweza kukabiliana na tatizo kubwa la wagonjwa ambao ni wengi katika hospitali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limekuwepo tatizo la watumishi. Karibu nchi nzima kumekuwa na kilio kwamba watumishi hawatoshi, sasa kutokana na tatizo hili la vyeti lililojitokeza tatizo la watumishi litakuwa ni kubwa sana. Kwa hiyo naomba Serikali ijipange haraka iwezekanavyo kuhakikisha inapeleka watumishi wa afya katika Wilaya zetu na hususani huko vijijini, la sivyo wananchi watapoteza maisha kwa wingi sana kwa sababu hakutakuwa na Wauguzi na Madaktari. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ijipange kuhakikisha watumishi wanapelekwa katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ilani yetu ya CCM tulisema tutajenga zahanati pamoja na vituo vya afya na wananchi kwa kushirikiana na Serikali wameshajenga maboma ya zahanati na vituo vya afya. Hata hivyo kumekuwa na kilio cha muda mrefu kwa ajili ya maboma yale, kwamba, yanabomoka na hayana msaada wowote. Kwa hiyo, naomba Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI waweze kuliangalia hili ili yale maboma yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi na Serikali kwa maaana ya zahanati na vituo vya afya yaweze kukamilika kusudi huduma…

KUHUSU UTARATIBU....
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nashukuru kwa kumwelimisha huyu ni Mbunge mgeni mimi ni senior. Naomba niendelee na mchango wangu. Naamini Wizara ya Afya pamoja na Wizara ya TAMISEMI wakikaa pamoja tutafanikiwa kuweza kupata majengo ya zahanati na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu Maendeleo ya Jamii. Maendeleo ya Jamii yamesahaulilka, nakumbuka siku za nyuma, enzi za mwalimu Mabibi Afya walikuwa wanatembea katika vijiji kuhamasisha shughuli za maendeleo na wananchi walikuwa wanaelimika kwa kupitia mabibi maendeleo. Sasa naomba kwamba maendeleo ya jamii wapewe vitendea kazi, tofauti na sasa hivi wako chini ya Mkurugenzi, Mkurugenzi akipata makusanyo ndipo anawapatia pesa kidogo ndio wanakwenda kufanya uhamasishaji wa shughuli za maendeleo vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, kwa kutumia Bunge lako Tukufu niwapongeze wa Wakurugenzi wa Wilaya ya Kasulu, Kibondo na maeneo mengine ya Mkoa wa Kigoma kwa kuweza kutimiza kwa kupeleka asilimia tano kwa vijana na wanawake. Kwa sababu hiyo, naomba sasa juhudi ziongezeke kusudi pesa hizo ziwe zinapelekwa kuweza kuwasaidia wanawake na vijana. Na watasaidiwaje basi, ni kwa kuungana na watendaji pamoja na hawa watu wa Maendeleo ya Jamii kwenda kuhamasisha wanawake na vijana kuanzisha vikundi ili ile asilimia tano inayotolewa ya vijana na wanawake iweze kupelekwa kwenye vikundi hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwamba tunafahamu kabisa vipo vituo vipya vya afya ambayo vinajengwa ambavyo kwa sasa hivi kwa mfano kule Wilaya ya Kasulu vipo vituo vipyaa vinavyojengwa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi mvua za kwanza ni za kupandia. Hivyo basi naomba Serikali iwe inawafikishia wakulima mbolea ya kupandia mapema kabla ya mvua za mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo mawakala waliofanya kazi ya kusambazia wakulima mbolea na mpaka sasa hawajalipwa pesa yao. Kwa vile Serikali ilishafanya uhakiki, kwa vyovyote ilishabaini ukweli uko wapi. Hivyo, naomba wale waliofanya kazi kwa uaminifu waweze kulipwa na wale waliodanganya wasilipwe, wengi wanapoteza maisha yao kwa sababu ya kudaiwa na mabenki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kusema hivi napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri wanayofanya, wakati anapanga kununua ndege watu hatukuweza kuelewa alikuwa ana maana gani, lakini sasa baada ya ndege zile kuwa zimefika na zimeanza kazi tayari tumeshaona alikuwa ana maana gani. Tunamshukuru Rais hasa sisi watu wa Kigoma, ndege zile zimeongeza utalii katika Mkoa wetu wa Kigoma, kwa sababu usafiri upo mara kwa mara watalii wanaenda Kigoma, kwa hiyo watalii wanaongeza pato kwa kupitia ndege zile wanazozitumia zisingekuwepo tusingeweza kunufaika kupata watalii wanaoweza kutalii katika Hifadhi za Gombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizugungumzie kuhusu matatizo ya mara kwa mara yanayohusiana na ongezeko la watu na ardhi kutokuongezeka. Asilimia kubwa ya Watanzania wengi ni wakulima na hasa akina mama sasa kutokana na jinsi watu wanavyoongezeka na ardhi ni ile ile kumekuwepo na matatizo mengi yanayotokea mara kwa mara. Serikali kwa kupitia watu wa TFS wanagombana na wananchi kwa sababu wananchi wanapokuwa wanaenda kulima kwenye maeneo wanafukuzwa wasilime kwenye maeneo yale kwa sababu mipaka haijaweza kuonyesha wananchi wanalima wapi na mipaka ya hifadhi ni ipi.

Kwa hiyo, nilikuwa ninamuomba Mheshimiwa Waziri kwa sababu hiki ni kilio cha muda mrefu, Mheshimiwa Waziri mimi ni Mbunge zaidi ya miaka kumi niko ndani ya Bunge hili na mara kwa mara tumekuwa tukitoa kilio chetu kuhusu Misitu ya Hifadhi kubaki haijawekewa mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa ninaomba kwa sababu Waziri wa Ardhi alisimama humu ndani akasema kwamba itaundwa tume na tume tayari iliishaundwa ikaanza kupitapita maeneo mbalimbali, kwanza nilitaka kujua je,majibu ya tume hiyo baada ya kuwa imezunguka maeneo mbalimbali yamefikia wapi? Kwa sababu majibu yakiishapatikana hayo sasa yatatoa majawabu ya kuweza kutenganisha ardhi ambayo wakulima watalima na ardhi ambayo itakuwa ni hifadhi kwa ajili ya Mapori Tengefu na Mapori Mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Kasulu, Kakonko na Kibondo wananchi wameendelea kupata taabu sana, kila wanapoenda kulima mashamba yao ambayo yamepakana na misitu ya Makele na Pori la Moyowosi wanapata shida sana wanafukuzwa, wanakimbizwa na hata katika maeneo mengine. Nilimsikia Mheshimiwa Sakaya akisemaa kule kwao Kaliua nyumba zimechomwa na hata wakati mwingine kule kwetu Kigoma nyumba zinachomwa, wanawake wanapata shida, watoto wanateseka, mazao yanachomwa, mavazi yanachomwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tulikuwa tunaomba Serikali iweze kutusaidia kufanya haraka na kutathmini maeneo hayo ili wananchi wapate maeneo ya kulima kwa sababu wananchi wanaongezeka, ardhi ni ile ile, lakini kwa sasa hivi wananchi wamekuwa na mwamko sana wa kuweza kutaka kulima na hata sisi Wabunge humu ndani. Wabunge walio wengi sasa hivi wameshika maeneo mengi wanataka kulima.

Kwa hiyo, tunaomba kabisa Serikali ifanye haraka iweze kupima maeneo hayo, iweze kuweka mipaka kusudi isogeze mipaka wananchi wapate maeneo ya kuweza kulima ili waweze kuinua kipato chao kwa kutumia maeneo ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeshuhudia maeneo mengi wakulima na wafugaji wanapigana, wanauana, vifo vimekuwa vingi kwa sababu ya kugombania mipaka, tulikuwa tunaomba Serikali ifanye haraka kuweza kubaini maeneo ya wakulima na wafugaji; na itenganishe mapema kusudi matatizo haya yanayotokea mara kwa mara ya watu kuuwana, kupigana mapanga na mikuki yaweze kumalizika mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahamasisha wananchi waweze kujitegemea, watajitegemeaje kama hawana maeneo ya kulima; na ndio maana mimi eneo langu kubwa ntakalolisemea leo hii ni kilio kikubwa cha kuiomba Serikali, Wizara ya Ardhi na Wizara ya Maliasili waweze kukaa pamoja kumaliza zoezi lile ambalo tayari waliishalianza waweze kutoa majibu ili Serikali sasa iweze kubainisha maeneo haya ya wakulima yawe ni haya ya wafugaji yawe ni haya na maeneo tengefu ya Serikali na yale yanayopakana na vijiji yaweze kujulikana ili kuwaondolea usumbufu wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wetu wanateseka sana hasa wanapokwenda kulima mashambani huko. Wanaondolewa kwa kupigwa, wananyang’anywa baiskeli, mazao yakiiva wanashindwa jinsi ya kwenda kuvuna. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninakuomba na ninakusihi sana, ninafahamu faida ya misitu lakini binadamu nao vilevile wanahitaji kunufaika kupitia misitu inayowazunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tulioupokea ushauri wako uliosema kwamba tuwafundishe watu jinsi ya kufuga nyuki na kutengeneza mabwawa ya samaki. Lakini hawataishi kwa kuvua samaki tu, watahitaji kupata mahindi kwa ajili ya ugali, watahitaj kupata maharage na mboga nyingine zinazotokana na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi ya kwangu leo yalikuwa ni hayo. Naiomba Serikali kwa mara nyingine tena, iwasaidie wananchi wa Wilaya ya Kasulu, wanaopakana na Kagera Nkandu.

MheshimiwaMwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba niipongeze Serikali ya awamu ya tano kwa jinsi inavyofanya kazi vizuri, na Serikali hiyo inayoongozwa na Mheshimiwa John Pombe Magufuli na kama anavyosema sisi Watanzania tuendelee kumuombea na kweli sisi tunamwombea Mwenyezi Mungu amjalie afya ili aweze kuendelea kuwatumikia Watanzania. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuendelea na hotuba yangu naomba niunge mkono hotuba hii kwa ajili ya wanawake wa Tanzania. Naomba niunge mkono hotuba hii kwa ajili ya wanawake wa Mkoa wa Kigoma na Wilaya zake zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naunga mkono bajeti hii? Wakati naunga mkono bajeti hii, naomba bajeti hii iongezewe pesa ili iweze kumkomboa mwanamke wa Tanzania kwa kumpatia maji. Tusipojipanga kuongeza bajeti hii, tujipange kuja na bajeti ya dharura ya kutibu kipindupindu. Kwa maana hiyo, naomba pesa ziongezwe kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme yafuatayo:-

Naishukuru Serikali kwa sababu mwaka 2016/2017 ilitupangia pesa Mkoa wa Kigoma, nawashukuru kwa hilo. Naomba niseme, pamoja na pesa hizo zilizopangwa, bado lipo tatizo la maji. Kwa hiyo, naendelea kusisitiza kwamba pesa zikipangwa zipelekwe ili kuweza kukamilisha miradi iliyokwishaanzishwa katika Mkoa wa Kigoma. Nimeona wakati Waziri anatoa hotuba yake amesema tumepangiwa pesa nyingine, namwomba Mheshimiwa Waziri pesa hizo zipelekwe ili kuweza kukamilisha miradi iliyopo Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, maji ni uhai. Sisi wote tunafahamu maji ni uhai na maji ni kila kitu. Kwa hiyo, naomba bajeti hii iongezewe pesa kwa sababu wanawake wanapojifungua wanahitaji maji. Wanawake pamoja na watu wengine wanaotunza familia; zipo familia ambazo zina wagonjwa wanaohitaji kutumia maji na wanatumia muda mwingi kwenda kutafuta maji. Wakati mwingine wanatafuta maji na wanakosa muda wa kwenda kufanya shughuli za ujasiriamali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, maji ni kila kitu. Maji yanachangia wananchi kuweza kuongeza kipato chao. Kwa mfano, sasa hivi tunahamasisha vikundi, wanawake waanzishe vikundi. Wakitumia muda mwingi kwenda kutafuta maji, watashindwa kufanya shughuli za uzalishaji na watashindwa kujiunga kwenye vikundi na hata wakijiunga hawataweza kurejesha mikopo katika vikundi vyao kwa sababu muda mwingi watakuwa wanautumia kwenda kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upo mpango wa kutafuta maji kutoka Mto Malagarasi. Kwa sasa hivi, maji katika Mto Malagarasi yanapungua na vyanzo vingi vinaendelea kuharibika kwa sababu wafugaji wanapeleka mifugo kwenye vyanzo vya maji. Naomba basi tunapopanga bajeti kwa ajili ya kupeleka maji vijijini tupeleke na pesa kwa ajili ya kwenda kuhamasisha wananchi kutunza mazingira kwa ajili ya kuhifadhi misitu ili maji yasipotee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mipango mizuri ya kutoa maji Mto Malagarasi lakini tusisahau kufanya mipango ya kutumia Ziwa Tanganyika, kwa sababu Ziwa Tanganyika ni ziwa kubwa ambalo linaweza likasambaza maji maeneo mengi. Maji hayo yakisambazwa katika maeneo mbalimbali, tutafanikiwa katika kilimo cha umwagiliaji. Kwa maana hiyo, Tanzania yenye viwanda itawezekana kwa sababu wananchi watakuwa wanazalisha mazao yao na kupelekea viwanda kuanzishwa kwa sababu vitu ambavyo vitakuwa vimelimwa kutoka mashambani vitakuwa vinapatikana kutokana na kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ipeleke pesa hizo ili kuweza kukamilisha miradi katika Mji wa Kasulu na viunga vyake ambako bado kuna maeneo yana matatizo ya maji. Mji wa Kibondo nao unahitaji pesa kwa ajili ya kukamilisha miradi ya maji. Vile vile Mji wa Kakonko unahitaji pesa. Kwa mfano, upo mradi mkubwa wa Mgembezi ambapo mradi huo ukikamilika utaweza kuhudumia Kata karibu tano. Kwa mfano Kata ya Kasuga, Kata ya Kakonko, Kata ya Kanyonza, Kata ya Kiziguzigu na Kata ya Kasanda. Kwa hiyo, tunaomba kabisa pesa hizo zikipatikana zielekezwe huko kwenda kukamilisha miradi ambayo tayari imeshaanzishwa. Ipo miradi mingine iliyoanza kutoka miaka takriban mitano hadi kumi, lakini bado haijaweza kukamilika. Tunaomba pesa zikipatikana zipelekwe zikakamilishe miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iongeze bajeti kwa ajili ya Wizara ya Maji ili tuweze kupeleka maji katika maeneo mbalimbali kumsaidia mwanamke wa Tanzania aweze kupata maji na kumtua ndoo kichwani kama Mheshimiwa Rais wetu alivyoahidi. Nami naamini Rais wetu akiahidi, kwa sababu tumeona mambo mengi aliyoahidi, aliahidi ndege, tayari sasa hivi ndege zipo. Zamani ilikuwa ni shida kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma, lakini kwa ahadi aliyoahidi, sasa hivi bombardier inaenda Kigoma, inaenda Tabora na maeneo mengine. Kwa maana hiyo, naamini hata tatizo la maji litakwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno hayo, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kusema hivi, CCM ni ileile, Mawaziri ni walewale, Wabunge ni walewale, Mheshimiwa Magufuli ni yuleyule na wananchi ni walewale. Sasa nasema hivi, wananchi wamejipanga vizuri kwa ajili ya kumuunga mkono Mheshimiwa John Pombe Magufuli. Kwa maana hiyo, nimeimba kwa kusema, ningesema CCM ni ileile, kwa hiyo, tumejipanga kuhakikisha 2020 hakitoki kitu. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kuunga mkono bajeti hii na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kaka yangu, Mheshimiwa Dokta Mpango na Naibu wake pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara ya Fedha kwa bajeti yao nzuri. Naomba niunge mkono mapendekezo yote ya Kamati ya Bajeti ya tozo ya Sh.40/=. Mapendekezo yao ni mazuri, nayaunga mkono kwa asilimia 100 kwa sababu yatakwenda kumwondolea mwanamke adha ya ndoo kichwani. Kwa hiyo, bajeti hii ni nzuri na mapendekezo ya Kamati ni mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa tozo hiyo ya Sh.40 pesa zile ziweze kupelekwa kwa ajili ya maji vijijini. Wananchi wanapata shida sana ya maji kule vijijini, wanawake hawawezi kufanya shughuli za maendeleo kwa sababu ya shida ya maji, lakini pesa hizo zikigawanywa zikapelekwa kule kwenye maji kwa kweli…

TAARIFA....

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa vile analitambua hilo na mimi nilisema Mheshimiwa Magufuli ni yuleyule kwa sababu hata ule wimbo wa CCM unasema Magufuli ni yuleyule. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naendelea, wananifahamu kwa sababu niliwahi kuwaambia Wapinzani Kigoma hawatarudi na tuliwafuta wote wakabakia wawili. Kwa hiyo, wale waliosalia nafikiri wanajua kazi yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kutenga asilimia 69 kwa ajili ya zahanati na vituo vya afya ili pesa hizo ziweze kwenda kumalizia miradi ile ya vile vituo vya afya na zahanati ambavyo wananchi kwa nguvu zao walianza kujenga. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali kwa kutenga pesa hizo shilingi bilioni 69 kwa ajili ya kwenda kusaidia miradi hiyo. Pesa hizo zikipelekwa kule wanawake watanufaika kwa sababu hawatapata shida sana kwenda kuvifuata vituo vya afya au zahanati maeneo ya mbali kwenda kutibiwa. Kwa maana hiyo, vifo vya wanawake na watoto vitapungua kwa sababu huduma zitakwenda kupatikana karibu. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali yangu inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka jana Mkoa wa Kigoma ulikuwa kati ya mikoa maskini na ilikuwa ni kwa sababu ya miundombinu ambayo haikuwa mizuri lakini naishukuru sana Serikali kwa sababu imeendelea kuutupia macho Mkoa wa Kigoma. Naomba pesa zilizotengwa kwa ajili ya barabara ya kutoka Nyakanazi kwenda Kanyonza, kutoka Kidahwe kwenda Kasulu, zipelekwe kwa ajili ya kwenda kumalizia barabara ile na ikibidi barabara ile yote iweze kumalizika kwa sababu ya kuunganishwa na Mikoa mingine ya Kagera na Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mkoa wa Kigoma ni wachapakazi sana, kwa hiyo miundombinu ikiwa mizuri kwa sababu ni wakulima wataweza kusafirisha vyakula vyao kwenda sokoni na tutawahamasisha wawekezaji waje kujenga viwanda ili wananchi wanapokuwa wanalima mazao yao waweze kupeleka kwenye viwanda ambavyo vitakuwa viko jirani na maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, sisi tumejaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji, tuna Mto Malagarasi, Mto Lwiche na Ziwa Tanganyika. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iweze kumalizia miundombinu ile ili wawekezaji waweze kuja kufanya kilimo cha umwagiliaji tuweze kuwa na viwanda vya sukari na kukamua mawese. Kwa hiyo, tunaishukuru sana Serikali kwa kuendelea kuutupia macho Mkoa wa Kigoma kwa ajili ya kuweka miundombinu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru kwa kuendelea kuuona Mkoa wa Kigoma, ndege zile za bombardier zinaenda Kigoma. Naomba sasa, reli ile inayojengwa ya standard gauge ianzie Dar es Salaam mpaka Kigoma, nyote mnajua reli ile ilikuwa inaanzia Kigoma kwenda Dar es Salaam, Dar es Salaam kwenda Kigoma, ndiyo maana inaitwa mwisho wa reli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba inapokuwa inafanywa mipango kuelekea Mwanza, chondechonde, tunaomba reli ile ije Kigoma. Kigoma mnaifahamu, tumepakana na DRC na Burundi, kwa hiyo, mkituwekea reli hiyo ya standard gauge hatutapata shida sana, tutaweza kuendelea kufanya biashara kwa kushirikiana na nchi hizo jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali na naipongeza kwa mipango ya umeme. Kwa hiyo, naomba pesa zipelekwe kwa ajili ya umeme wa REA awamu ya tatu ili pesa zikipatikana ziweze kuja Kigoma kwa ajili ya kuweka umeme katika vijiji vyetu vinavyozunguka miji yetu katika Miji ya Kibondo, Kakonko, Kasulu, Uvinza, Buhigwe na maeneo mengine yote. Kwa hiyo, naomba REA iongezewe pesa kwa sababu baadhi ya vijiji havijaweza kupata umeme, pesa zikipatikana umeme utaweza kupatikana katika vijiji vyote vinavyozunguka miji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo malalamiko ya mawakala ambao wamefanya kazi ya kusambaza mbolea kwa wananchi. Nafahamu wapo mawakala waliofanya kazi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa, naomba Serikali ijipange, wale ambao ni waaminifu walipwe pesa yao. Ni muda mrefu sasa wamesubiri, nyumba zao zimeuzwa, wengine wamekufa kwa sababu walikopa kwenye mabenki lakini wameshindwa kurejesha kwa sababu hawajapata pesa. Kwa hiyo, naomba ufanyike utaratibu wa kuweza kuwalipa ili waweze kurejesha madeni yao benki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, SACCOs na SACAs, tumekuwa tukiwahamasisha wananchi kuanzisha SACCOs na SACAs lakini upo upungufu mkubwa wa watumishi wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika. Wafanyakazi hao wa ushirika hawatoshi na vile vikundi vilivyoanzishwa vijijini kwa maana ya SACCOs na SACAs wanahitaji elimu, hawajui jinsi ya kukopa, hawajui jinsi ya kurejesha na hawajui ili wakopesheke ni lazima wakaguliwe na vyombo vinavyofanya kazi ya ukaguzi wa pesa ili kubaini kama hawa watu tukiwapa pesa wataweza kuirejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie eneo hili, watumishi wa ushirika hawapo kule vijijini na hata hao wachache waliopo hawana vitendea kazi. Kwa hiyo, tunaomba hawa watumishi wa ushirika, kwanza waajiriwe ili wawe wengi, lakini wapewe vitendea kazi ili waweze kwenda vijijini kuzifundisha SACCOs na SACAs zetu ziweze kuelewa vizuri, hatimaye tutakapopata pesa hata hizi asilimia 10 kwa maana ya wanawake na vijana zinapopelekwa kwenye vikundi wajue ni jinsi gani watatumia kwa sababu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri na ninampongeza Mheshimiwa Waziri Jenista, mwalimu wangu, mwalimu wa wangi lakini na Naibu Mawaziri pamoja na watendaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii vilevile kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya, mambo mengi aliyoyaahidi mwaka 2015 tumeona yakiendela kutekelezeka. Aliahidi ndege zitakuja na tumeshuhudia zikija, kwa kweli tunamshukuru sana.

Nashukuru pia kwa mambo yanayoendelea kutendeka katika Mkoa wa Kigoma. Tunashukuru sana kwa miradi ya barabara inayoendelea. Kwa hiyo, ninashukuru sana na ninaomba tuendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia mara nyingi hata anapofanya ziara zake mbalimbali anasikiliza matatizo ya watu na kuyapatia majibu pale pale. Mwaka jana alikuja katika Wilaya ya Kasulu, kulikuwa na kilio kikubwa cha muda mrefu wananchi walikuwa wakililia Hifadhi ya Kagera Nkanda akayatolea majibu pale pale. Wananchi wa Wilaya ya Kasulu wanafurahi, sasa hivi wanalima, wanazalisha mahindi na maharage. Kwa hiyo, wanaendelea kumshukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la maji. Nchi yetu imejaaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji ikiwemo bahari, maziwa, mito mikubwa na midogo lakini bado tuna tatizo kubwa la maji. Nilikuwa ninaiomba Serikali kwa kutumia vyanzo hivyo ambavyo tulijaaliwa na Mwenyezi Mungu iweze kuhakikisha maji yanafika vijijini. Wanawake muda mwingi wanatumia nafasi ya kwenda kutafuta maji badala ya kutumia nafasi hiyo katika uzalishaji mali. Kwa hiyo, naomba maji yaweze kufikishwa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Kasulu hususan Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Vijijini bado kuna tatizo kubwa la maji na katika Mkoa mzima wa Kigoma bado kuna matatizo ya maji, Kibondo, Kakonko na maeneo mengine yote. Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba maji Kigoma yaweze kufika. Katika Wilaya ya Kasulu viko vijiji ambavyo vinapakana kabisa na Mto Malagarasi lakini kwa bahati mbaya vijiji hivyo havina maji. Naomba Kijiji cha Kitanga ambacho kiko mbali kabisa na kinapakana na Mto Malagarasi kiweze kupatiwa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwa kuweza kufanya watoto waende kusoma bila kulipa ada yoyote na tunamshukuru Rais kwa kuja na sera hiyo. Pamoja na hayo bado yapo matatizo madogo madogo, watoto wameenda shule, wamekuwa wengi, vyumba vya madarasa vimekuwa vichache, nyumba za walimu hazitoshi. Kwa hiyo, naomba kwa kusaidiana na wananchi, Serikali iweze kuhakikisha madarasa yanajengwa ili watoto wetu waweze kupata sehemu ya kusomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe ombi hapa, ipo shule moja ambayo kutoka Kasulu Mjini kuelekea katika kijiji hicho ni kilometa zaidi ya 100 na kijiji hicho hakina sekondari ya kata. Ili watoto waweze kupata elimu, wanatembea kilometa 50 kutoka Kitanga kwenda Helushingo kwenda kutafuta elimu ya sekondari. Kwa vile wananchi walishaonesha bidii ya kufyatua tofali na kuanza kujenga, naomba sasa Serikali iangalie ni jinsi gani itawasaidia ili waweze kukamilisha vyumba vya madarasa wanafunzi waweze kupata madarasa ya kusomea na waepukane na safari ndefu ya kwenda kutafuta elimu katika Kata ya Helushingo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimpongeze Profesa Ndalichako, amekuwa akifanya ziara nchi nzima na tumeshuhudia ziara zake zimezaa matunda, pale alipopita madarasa yameboreshwa na ninamshukuru hata Kigoma Sekondari imeweza kunufaika na ziara zake, lakini na Chuo cha Ualimu Kasulu nacho kimeweza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nishukuru Mawaziri wote, ziara wanazozifanya kwa kweli, wanakopita huku na kule tunaweza kunufaika. Mwaka jana Mheshimiwa Ummy alizunguka katika Mkoa wa Kigoma tuliweza kunufaika tukapata magari nane kwa ajili ya Wilaya zote za Mkoa wa Kigoma. Kwa hiyo, ninaendelea kuwapongeza Mawaziri kwa ziara zao. Bado tunalo tatizo la watumishi katika vituo vya afya, katika zahanati na hata katika hospitali za Wilaya. Kwa mfano katika hospitali ya Wilaya ya Kasulu, wauguzi hawatoshi, waganga hawatoshi. Nurse mmoja anaweza akahudumia wodi moja akiwa yeye peke yake amuwekee mgonjwa maji, ahangaike kwenda kupima temperature, kwa kweli tunaomba Serikali iongeze watumishi katika hospitali ya Wilaya ya Kasulu na hata katika hospitali nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru Wilaya mpya zile za Buhigwe na Kakonko nimeona tulitengewa shilingi milioni 500 katika Wilaya ya Buhigwe zimekwenda na hospitali ninaamini itaanza kujengwa, lakini na Kakonko zilishaanza kupelekwa kidogo kidogo. Ninaomba basi, pesa zilizosalia zipelekwe ili tuweze kupata hospitali katika Wilaya ya Kakonko na Wilaya ya Buhigwe ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Uvinza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wahamiaji haramu na wakimbizi; Mkoa wa Kigoma umapakana na nchi ya Burundi na DRC, kuna wimbi kubwa la wakimbizi wanaoingia wengine kihalali kwa kuletwa kwa sababu wanakuwa wameingia wakati ule wa vita na wengine ambao wanapita njia ya panya, kwa hiyo, Mkoa ule una wakimbizi wengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mfano halisi, Kijiji cha Kitanga wanaingia wakimbizi wengi sana. Kwa mfano, pesa hizi zinazotolewa kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye maisha duni, pesa zinazotolewa na TASAF, wakimbizi ndio wanaonufaika. Nimeshuhudia wakimbizi 70 wakipewa pesa za TASAF wakati wananchi wa Tanzania hawapati pesa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kulalamika kuhusu wakimbizi wanaoingia Kitanga, lakini mpaka sasa hivi bado wakimbizi wanaingia. Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi ninaomba kabisa kule Kitanga mtupie macho kule kwa sababu, wakimbizi wanaingia kwa wingi na ndio hao wanaoendelea kunufaika kwa kupata pesa hizo za TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa naomba niongelee kuhusu uwezeshwaji, jana nimeongea nilipokuwa ninauliza swali la nyongeza. Ninamuomba Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa sababu kule Kigoma tayari kuna vikundi vingi, kuna SACCOS nyingi, ninaomba basi kwa sababu mikoa mingine ilishafikiwa na mifuko ile ya uwezeshaji, naomba safari hii katika bajeti hii Mheshimiwa Jenista Mhagama macho yako uelekeze mkoani Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo ninaomba nishukuru, ahsante sana na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Ummy kwa hotuba yake nzuri, nimpongeze Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Afya. Nampongeza sana Mheshimiwa Ummy kwa sababu ni ukweli usiofichika kwa jinsi anavyofanya kazi kubwa ya kuhakikisha vifo vya akina mama na watoto vinamalizika, ninampongeza sana. Tumeendelea kuona anavyofanya kazi katika nchi yetu ya Tanzania, anavyofanya ziara katika maeneo mbalimbali, kwa kweli ziara zake anazozifanya zinazaa matunda, tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweza kushuhudia jinsi theatres zinavyojengwa, vituo vya afya, wodi za wazazi zinavyojengwa, sasa baada ya juhudi hizo kinachofuata sasa tunaomba ahakikishe wanapatikana wataalam wa kuweza kufanya shughuli hiyo ya kuwasaidia akina mama kwa sababu maeneo mengi hakuna madaktari, hakuna waganga wa upasuaji. Kwa hiyo, tunaomba wataalam hao baada ya kuwa theatres zimejengwa, baada ya kuwa wodi zimejengwa, waweze kupatikana wataalam wa upasuaji. Tusipofanya hivyo akina mama wengi watapoteza maisha kwa sababu maeneo hayo wasipopelekwa wataalam watakuwa wanafanya upasuaji watu wasiokuwa na ujuzi matokeo yake badala ya kunusuru maisha ya akina mama wataweza kufa kwa wingi.

Kwa hiyo, ninaiomba Serikali ihakikishe madaktari na wataalam wanapelekwa katika theatres hizo zinazojengwa pamoja na wodi hizo zinazojengwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nizungumzie Mkoa wa Kigoma; Mkoa wa Kigoma karibu asilimia 65 hatuna watumishi kabisa. Ninaomba basi kwa sababu muda mrefu Mkoa wa Kigoma kutokana na miundombinu haikuwa mizuri barabara tulikuwa hatuna, reli ilikuwa inasuasua, watumishi walikuwa wakipangiwa Kigoma hawaendi, lakini sasa baada ya Mkoa wa Kigoma kuanza kufunguka tunaomba wataalam waweze kupelekwa Kigoma ili tuweze kupata watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika Hospitali ya Kasulu tuna madaktari wanne na mahitaji ya madaktari ni 23, kwa hiyo tuna upungufu wa madaktari 19. Lakini wapo Madaktari Wasaidizi, mahitaji ni 35 lakini tunao wanne, pungufu 31 na ma-nurse pamoja na wauguzi kwa kweli hawatoshi, tunaomba mtusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Kibondo kama nilivyoeleza wiki iliyopita wakati nauliza swali la nyongeza. Mkoa wetu wa Kigoma kuna wakimbizi, wakimbizi wanaotoka katika maeneo mbalimbali ya makambi ya wakimbizi wengine wanapelekwa katika Hospitali ya Kibondo, kwa hiyo, tunahitaji watumishi waweze kuongezwa katika Hospitali ya Kibondo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Kakonko ni Wilaya mpya hakuna Hospitali ya Wilaya na wagonjwa ni wengi kwa sababu Wilaya ile inapakana na Mkoa wa Kagera, wapo wagonjwa wengine wanaotoka mkoa wa jirani kuja kutibiwa katika kituo kile cha Kakonko, tunaomba Serikali ihakikishe Hospitali ya Wilaya ya Kakonko inamalizika haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hilo la hospitali lililopo Kibondo na Kakonko ni hivyohivyo. Katika Kituo cha Mtendeli cha Wakimbizi, wakimbizi wanatoka kuja kutibiwa katika Kituo cha Afya cha Kakonko, kwa hiyo, naiomba Serikali ihakikishe Hospitali ya Wilaya ya Kakonko inajengwa haraka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza napenda niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa jinsi inavyofanya kazi. Naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mheshimiwa January Makamba, Naibu wake, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii kwa hotuba waliyotuletea leo hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitazungumzia kuhusu mazingira. Kuanzia 1995, Mkoa wa Kigoma ulipata na wimbi kubwa la wakimbizi lakini pamoja na Mikoa ya jirani ikiwemo Kagera na Rukwa. Kutokana na wimbi kubwa la wakimbizi kufika katika mikoa hiyo ni ukweli usiopingika yametokea madhara makubwa ya uharibifu wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walipoingia watu kutoka Burundi kwa mara ya kwanza katika Wilaya ya Kasulu walifikia katika Kambi moja ya Mtabila, wakati huo mazingira yaliharibika kwani miti mingi ilikatwa. Kwa hiyo, unaweza kuona ni jinsi gani mazingira yalivyoweza kuharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata waliporudishwa walienda tena kwenye Kambi moja ya Nyarugusu ambayo ni kubwa, ina wakimbizi wa kutoka DRC na Warundi. Kwa hiyo, ni jinsi gani unaweza kuona mazingira katika Mkoa wa Kigoma yalivyoharibika na kule Kibondo vilevile ipo Kambi ya Nduta lakini Kakonko iko Kambi ya Mtendeli. Kwa hiyo, naiomba Serikali kwa kushirikiana na Shirika la UNHCR kuangalia ni jinsi gani zinaletwa pesa kwa ajili ya kunusuru mazingira katika mikoa hiyo ambayo ilipokea wakimbizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naiomba Serikali iweze kuipatia Ofisi ya Makamu wa Rais pesa za kutosha kwa ajili ya kuweza kufanya ziara katika mikoa hiyo lakini kuweza kupeleka pesa kwa ajili ya kukabiliana na tatizo hili la mazingira. Ukienda kuangalia jinsi misitu ilivyoteketea, kwa kweli ni kilio kikubwa sana na wakati mwingine uharibifu wa mazingira unaendelea siyo kwamba eti mazingira yanahifadhiwa, hapana. Bado tuna kila sababu ya kuhakikisha Wizara hiyo inapatiwa pesa ili kwenda kunusuru mikoa ile ambayo imeathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Muungano, naomba wanafunzi waendelee kufundishwa umuhimu wa Muungano kuanzia darasa la kwanza mpaka vyuo vikuu. Kwa sababu watoto wakianza kufundishwa wakiwa bado ni watoto wataendelea kuupenda tangu mwanzo mpaka watakapoendelea kuwa wakubwa na wataendelea kuulinda kwa nguvu zao zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia rehema za kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hoja. Napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Profesa Mbarawa kwa hotuba yake nzuri. Niwapongeze Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Kwandikwa na kaka yangu Mheshimiwa Nditiye na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa juhudi zake anazoendelea kuwatumikia Watanzania bila kuchoka. Nafurahi kila ninapomwona anapofanya ziara anapotatua matatizo ya wanawake wanaokuwa wamemtolea matatizo pale kwenye ziara, anapoyatolea majibu pale pale, kwa kweli huwa nafarajika sana kama mwanamke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Barabara ya Kidawe –Kasulu - Nyakanazi-Kabingo. Sisi watu wa Kigoma ukisimama usizungumzie barabara hiyo unakuwa hujajitendea haki wewe mwenyewe, lakini unakuwa hujawatendea haki wananchi wa Mkoa wa Kigoma. Kwa muda mrefu sana wananchi wa Mkoa wa Kigoma wanapata shida sana, barabara hiyo haipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kipindi hiki cha mvua mwezi wa Tatu na wa Nne, mvua ilikuwa inanyesha kila siku iendayo kwa Mungu na magari yalikuwa hayapiti, likipita gari moja kubwa likikatisha barabara msururu wa magari kama 20 unafata nyuma akinamama na watoto wanapata shida sana. Ndio maana ninaposimama hapa jioni hii ya leo naomba Serikali iendelee kuweka juhudi za kuhakikisha barabara hiyo inakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nyakanazi- Kabingo mkandarasi alishapewa pesa, lakini hajaweza kumaliza kukamilisha barabara hiyo. Nakumbuka mwaka jana Rais alipokuja Kigoma mkandarasi alileta vifaa vyake vingi vya maonyesho kuonyesha kama yupo kazini, lakini alipoondoka Mheshimiwa Rais zile juhudi zikaishia palepale. Naomba basi kwa vile ameshapewa pesa na pesa yake amekamilishiwa tunaomba barabara hiyo iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, barabara ya Kidahwe - Kasulu mkandarasi alikuwa hajakamilishiwa malipo yake akawa amesimama kuweza kujenga barabara hiyo, lakini kwa sasa ameanza, naomba naye aendelee kuhimizwa ili aweze kumaliza kazi hiyo na apelekewe pesa kusudi barabara hiyo iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa mazungumzo ambayo tayari wameshaanza na Benki ya ADB, naomba juhudi zifanyike. Barabara hiyo inapita katika misitu minene ukizingatia kwamba Mkoa wetu wa Kigoma umekumbwa na wimbi kubwa la wakimbizi. Wakimbizi wanapelekwa katika Mkoa wetu wa Kigoma, sasa usalama ni wa mashaka kwa sababu watu wote ambao sio waadilifu wanaenda kujificha katika misitu hiyo wanafanya ujambazi na ni kwa nini? Kwa sababu barabara ile haipitiki kiurahisi, ndio maana wanapata nafasi ya kwenda kujificha pale kufanya uhalifu. Kwa hiyo, naomba juhudi zifanyike barabara hiyo iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishukuru kwa pesa ambazo zimetolewa na Falme za Kiarabu. Naomba zile kilometa 51 za kutoka Uvinza mpaka Malagarasi ziweze kufanya kazi zitakapopatikana ili kipande kile kiweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kipo kile kipande cha Chagu mpaka Kazilambwa, nacho naungana na Mheshimiwa Sakaya kipande kile ni kibaya sana. Wananchi wa Mkoa wa Kigoma hawana namna nyingine barabara zinapokuwa zimeharibika napengine inapotokea pengine usafiri wa treni umesitishwa, hakuna barabara nyingine wanayoitumia tofauti na barabara ya kupitia Uvinza - Tabora - Manyoni - Dar es Salaam. Kwa hiyo tunaomba barabara ile na yenyewe ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kigoma - Nyakanazi ndio barabara inayounganisha Mkoa wa Kigoma na mikoa ya jirani, kwa hiyo ni barabara muhimu sana, tunaomba barabara hiyo ikamilishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza juhudi za Serikali kwa kazi kubwa iliyokwishaanza ya standard gauge. Naomba isiishie Dodoma tu naomba ifike Tabora hadi Kigoma. Usafiri wa reli ni muhimu sana kwa wananchi wa Mkoa wa Kigoma na maeneo ya Kanda ya Ziwa. Kwa hiyo, tunaomba standard gauge napo Kigoma iweze kufika kwa sababu nyie wenyewe humu ndani huwa mnatutania Kigoma mwisho wa reli. Kwa hiyo, tunaomba ianzie kule kule ambako ndio kuna historia. Reli ikikamilika wananchi watapata nafasi ya kusafiri kwa gharama nafuu na itakuwa ni rahisi kusafirisha mizigo yao kuipeleka sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye mawasiliano ya mitandao ya simu. Mkoa wa Kigoma umepakana kabisa na nchi jirani za Burundi, DRC na Rwanda na wakati mwingine ukipiga simu kwa watu ambao wapo mipakani wanaitika watu wa nchi jirani. Tunaomba maeneo yale ambayo minara haipo Serikali iweze kufanya mazungumzo na watu wa mashirika wanaopeleka minara ili tuweze kupelekewa minara katika maeneo mbalimbali ili tuweze kupata mawasiliano bila shida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo kwangu ni hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Na mimi nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufufua viwanda vyetu hasa viwanda hivi vidogo vidogo ni lazima suala la kuwa na mashine au vitendea kazi na wataalam kutazamwa kwa macho mawili. Taasisi hii ya SIDO ndiyo taasisi yenye uwezo na taaluma ya kutengeneza mashine ndogo ndogo ambazo zinawasaidia wananchi wetu wenye kipato cha hali ya chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, ni lazima Serikali iimarishe na kufanya shughuli zake za kuhakikisha SIDO inaweza kuimarishwa kwa kupatiwa mtaji. Mara nyingi pesa zimekuwa zikitengwa kupelekwa SIDO, lakini zikawa haziendi. Kwa hiyo, naomba kabisa SIDO iweze kutizamwa kwa macho mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa SIDO haifanyi vizuri kwa sababu baadhi ya vitendea kazi kama mashine, zimepitwa na wakati. Haziwezi kufanya ushindani na mashine zinazotoka nchi za nje kwa sababu mashine zetu zilizopo sasa hivi ni zile za muda mrefu. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iweze kutoa pesa kusudi SIDO iweze kwenda sambamba na mashine zinazoingizwa kutoka nje ya nchi. Hivyo basi, naomba Serikali iweze kuhudumia SIDO na kuipa wataalamu wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naipongeza Serikali kwa kutambua umuhimu wa kuiimarisha SIDO. Katika ukurasa wa 143 wameandika ni jinsi gani watakavyohakikisha SIDO inaweza kuimarika na wamesema; “Kutumia SIDO kama nyenzo ya kujenga viwanda vidogo vidogo na vya kati kwa kuendelea kulifanyia maboresho shirika hilo la SIDO na kuhamasisha ubunifu na matumizi ya teknolojia.” Kwa hiyo, ninaomba sana kazi hiyo ya kuhakikisha SIDO inaimarishwa iweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka ni lazima maonesho yanakuwepo. Mara nyingi wananchi wa kutoka vijijini wanakuja kuonesha biashara zao kwenye maonesho lakini tatizo ni masoko. Kwa hiyo, naiomba Serikali ihakikishe inawaruhusu wanafanya maonesho, lakini itafute masoko

kwa sababu wanapokuwa wamepeleka kwenye maonesho wanakaguliwa halafu wanakosa maeneo ya kupeleka kuuza bidhaa zao, wanakata tamaa. Kwa hiyo, naiomba Serikali, sambamba na kufanya shughuli ile ya maonesho, lakini iweze kutafuta masoko kwa ajili ya wajasiriamali wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Mheshimiwa Zainab na Mheshimiwa Zitto Kabwe, katika Mkoa wa Kigoma tunalima zao la michikichi. Tunaiomba Serikali iweze kuja kuwekeza Kigoma ili tuweze kuanzisha viwanda vya mafuta na vilevile viwanda vya kutengeneza dawa kwa sababu zao la michikichi linatoa mafuta, lakini vilevile linaweza likasaidia kuanzishwa viwanda vya dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikuwa nataka kuzungumzia uwekezaji wa kiwanda katika Wilaya ya Kasulu, Kijiji cha Kitanga. Aliwahi kuja mwekezaji, karibu miaka 10 iliyopita, akaja akaoneshwa eneo, tangu ameondoka hajaweza kurudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naiomba Serikali mpaka sasa hivi eneo hilo lililoko katika Kijiji cha Kitanga, bonde ambalo ni la Mto Malagarasi bado lipo, kwa hiyo, bado tunaihitaji Serikali iweze kututafutia mwekezaji katika bonde hilo ili aweze kulima kilimo cha miwa, lakini vilevile aweze kujenga kiwanda cha sukari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo tutaweza kuimarisha uchumi wetu na viwanda vitaweza kuongezeka. Ni lazima tuhakikishe tunawekeza katika kilimo ili viwanda viweze kupatikana kutokana na mazao ya kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamekuwa wakiogopa kuja Kigoma kwa sababu ya miundombinu, lakini naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri, kwa sasa hivi miundombinu Kigoma inaenda kuimarika, barabara zinajengwa, uwanja wa ndege wa Kigoma umetengenezwa na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa juhudi zake, ndege za bombardier zinakuja. Kwa hiyo, wawekezaji watakapokuwa wanakuja Kigoma, hawatapata shida kwa ajili ya kuja Kigoma kwa ajili ya kufanya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, naomba kuzungumzia ujenzi wa barabara ya Kigoma – Nyakanazi. Barabara hii imechukua muda mrefu sana lakini mpaka leo haijakamilika. Nomba Serikali iweze kusimamia ili iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, kipo kipande cha kutoka Uvinza – Malagalasi, nacho ni tatizo. Tunaomba kipande hiki nacho kiweze kujengwa. Kipo kipande cha Chagu - Kazilambura nacho tunaomba kiweze kujengwa ili wananchi waweze kuondokana na adha ya usafiri.

Mheshimiwa Spika, mwisho, naomba nishukuru Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuweza kukubali barabara ya kutoka Kabingo- Kibundo- Kasulu - Bulingwe kujengwa kwa lami kupitia fedha za AfDB.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia. Kwanza naomba niwapongeze Wenyeviti wote wawili kwa taarifa zao nzuri, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyojitabisha kwa ajili ya Watanzania, anafanya kazi usiku na mchana ili kuwaletea maendeleo Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kuhusu reli ya SGR, reli hii inakwenda sambamba na viwanda pamoja na kilimo, vitu vyote vinashabihiana. Naomba kushauri wakati tunaendelea na ujenzi wa reli, tuweze kulima mazao ya biashara lakini niishukuru Serikali kwa jinsi ilivyokuja na mpango wa kilimo wa mchikichi. Katika Mkoa wa Kigoma tukiwekeza katika kilimo cha mchikichi na huku reli ikiwa inajengwa, wakati reli ya SGR inakamilika, mazao yale ya mchikichi yatakuwa tayari yanaanza kustawi na kuvunwa na kupelekwa sokoni. Kwa hiyo, kupitia reli hiyo tutaweza kusafirisha mawese kupeleka katika viwanda. Hivyo, naipongeza Serikali kwa kwenda sambamba na mambo ya ujenzi wa miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niishukuru Serikali kwa kutoa pesa kwa ajili ya kujenga barabara kutoka Kankoko – Kibondo – Kasulu - Buhigwe naipongeza sana Serikali kwa kuweza kuliona hilo. Naomba wakati barabara hiyo imejengwa iweze kujengwa border post kwa ajili ya kusafirisha mizigo inayotoka Burundi kuja Tanzania ili waweze kufanya biashara kwa kushirikiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma umepakana na nchi jirani ya Kongo pamoja na Burundi na sisi Kigoma tunalima mahindi, maharage, mpunga pamoja na mihogo. Kwa hiyo border katika Mkoa wa Kigoma kwa maana ya Wilaya zote nne zimepakana na nchi jirani; ukienda Kakonko imepakana na Burundi, ukija Buhigwe imepakana na Burundi, lakini ukija Kigoma Vijijini nayo imepakana na nchi ya DRC. Kwa hiyo tunaomba boader iweze kujengwa ili wananchi wa pande zote mbili, wananchi wa Tanzania pamoja na wananchi wa kutoka Burundi na Kongo waweze kufanya biashara kwa kushirikiana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri, reli ya SGR iweze kuanzia Kigoma kabla ya kwenda Kigali kwa sababu mizigo mingi inatokea Burundi na Kongo na inapitia Kigoma. Kwa hiyo, naomba kabla ya kwenda kujenga Kigali, ianzie Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo linawasumbua sana wananchi wa Mkoa wa Kigoma. Mara nyingi watu wa Uhamiaji wamekuwa wakiwasumbua wafanyabiashara kwa kuweka vikwazo mbalimbali kwamba siyo Watanzania kitu ambacho kinawakatisha tamaa wananchi wakati mwingine wanashindwa kufanya biashara kwa uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba watu wa Uhamiaji waliangalie suala hili wasiwazuie wananchi kufanya biashara ila wawaelimishe waweze kujua ni jinsi gani wale watu ambao wapo mipakani wanaweza kufanya biashara kwa kushirikiana na nchi jirani. Tukiendelea kuwasumbua wananchi ambao wanatokea mipakani tutaendelea kupoteza mapato. Serikali haitaingiza mapato kwa sababu wananchi hawatatumia border watatumia vichochoro kwa ajili ya kuingiza biashara zao sokoni. Kwa hiyo, tutakuwa tumepoteza mapato kwa sababu ya kusumbuliwa na watu wa Uhamiaji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuruku kwa kunipa nafsi hii. Naomba niungane na wenzangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Kigwangalla pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Kanyasu, Katibu Mkuu na wafanyakazi wote wa Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naunga mkono hoja. Pia naomba niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweza kuruhusu baadhi ya maeneo ya wafugaji na wakulima waweze kupatiwa maeneo ya kulima na maeneo ya malisho.

Vilevile naomba niendelee kusema kwamba maeneo ya kilimo na malisho ya mifugo yameendelea kupungua kutokana na ongozeko kubwa na watu hivyo basi, unakuta eneo la kilimo halitoshi, lakini pia eneo la malisho ya mifugo haitoshi. Ombi langu, Serikali iweze kuridhia kupunguza eneo la hifadhi na maeneo ya akiba kurudi kwa wananchi ili waweze kupata maeneo ya kulima na maeneo ya kulishia mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali izingatie kauli ya Mheshimiwa Rais kwa kuweza kuendelea kutenga maeneo ya wafugaji na wakulima. Ukiangalia migogoro mingi iliyopo nchini ni kutokana na upungufu wa ardhi ya wananchi kulima lakini pia na malisho ya mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu Kasulu, Eneo la Akiba la Makere Kusini, bado kuna mgogoro mkubwa pamoja na kwamba Serikali imeongeza eneo kidogo, lakini bado wananchi wana mahitaji makubwa ya kupata eneo la kulima kwa sababu watu wameongezeka, ardhi inabaki kuwa ile ile naomba Serikali iweze kuruhusu kuongeza kipande kingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe watu wa TFS waache kuwasumbua wananchi, waendelee kuwaelimisha, kwa sababu nimeshawahi kusimama hapa kulalamika kuhusu watu wa TFS wanavyowasumbua wananchi. Naomba wawaelimishe kwa kukubaliana na kuwaelekeza jinsi gani wanatakiwa kufanya kuliko kuchukua wakati mwingine mali zao, kuchukua pikipiki wakachoma, wakati mwingine kuchua baiskeli zao. Wawaelimishe, wakae nao wakubaliane ili wote waweze kutoka kwa pamoja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama ndani ya Bunge lako na kuchangia hoja hii ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Kwanza napenda nimpongeze Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Katibu Mkuu - Dkt. Chaula kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipongeze kwa moyo wa dhati kabisa jinsi Serikali ya Awamu ya Tano inavyofanya kazi ya kujenga hospitali pamoja na vituo vya afya. Naomba nishukuru kwa moyo wa dhati kabisa kwa Serikali kuweza kusaidia Hospitali ya Maweni kwa kupeleka shilingi milioni 500 ili kuendelea kuimarisha hospitali ile ambayo inatumiwa na wananchi wote wa Mkoa wa Kigoma. Ahsante sana, tunaamini pesa hizo zikifika zitaendelea kukarabati hospitali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishukuru Serikali kwa kuweza kukubali kujenga Hospitali ya Wilaya ya Kakonko. Waziri Mkuu alipokuja alikubali kupeleka shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Kakonko na tayari shilingi milioni 500 zimepangwa kwa ajili ya kuanza ujenzi huo. Nashukuru kwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya Hospitali ya Kasulu DC, tayari fedha zimeshafika na tayari wameshaanza ujenzi. Nashukuru na ujenzi wa hospitali inayoendelea katika Wilaya ya Buhigwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia wakati huu vituo vya afya vinakarabatiwa na vingine vinajengwa, tunaishukuru sana Serikali. Naomba vituo hivyo vinavyojengwa ambavyo vipo tayari na vingine ambavyo bado viweze kupelekewa madaktari, wauguzi pamoja na vifaa tiba, sambamba na wataalamu wa dawa za usingizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi kwa Waziri wa Afya pamoja na Katibu Mkuu, kwa sababu wao ni akina mama, vipo vituo vingine karibu na hospitali ya wilaya lakini kuna maeneo mengine yapo mbali kabisa. Kwa mfano, kutoka Kasulu Mjini kwenda eneo moja la Kitanga ni kilometa 123 lakini hawana kituo cha afya. Lipo eneo lingine tena linaitwa Kagera Nkanda, kutoka Kasulu Mjini ni kilometa 78. Naomba kwa vile wao ni akina mama washirikiane na Waziri wa TAMISEMI kuona ni namna gani wanaweza kuwasaidia akina mama ambao wanaishi umbali mrefu sana na hawana vituo vya afya ili tuweze kupata vituo vya afya katika maeneo hayo ambayo yako mbali kutoka Wilaya ya Kasulu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile katika Wilaya ya Kakonko, Gwanuku wameshapata kituo cha afya lakini Mgunzu pamoja na eneo moja linaitwa Muhangi na wao wako mpakani hawana vituo vya afya. Naomba na wao waangaliwe kwa sababu wako mpakani waweze kupewa vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nilichotaka kuzungumzia, mara nyingi sana wananchi wanapoenda kutibiwa katika maeneo mbalimbali wakipangiwa kwenda maabara kupima hawezi kurudi bila kuambiwa kwamba hajapatikana na tatizo la UTI. Kila vipimo vinapotoka mgonjwa akipimwa ni lazima ataambiwa kwamba ana tatizo la UTI. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Ndugulile atueleze ni kwa nini wagonjwa walio wengi hasa vijijini na hata mijini hawawezi kutibiwa bila kuambiwa kwamba wana UTI? Ni kwa nini maeneo mengi wanapatikana na matatizo hayo? Nilitaka nijue ni vipimo gani vinavyotoa majibu mengi yanayofanana? Kwa sababu mimi napata wasiwasi isijekuwa kuna maeneo mengine watu wanaambiwa kwamba wana UTI kumbe watu wanafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wazee maeneo mengi wanalalamika kwa kutokupata huduma ya kutibiwa bure. Hiki kimekuwa ni kilio kikubwa cha wazee, maeneo mengi ukienda hata tunapoenda kwenye ziara wazee wengi wanatulalamikia kwamba Serikali ilisema itatoa huduma ya matibabu bure lakini bado huduma hiyo maeneo mengine hawajaweza kutibiwa bure. Yapo maeneo ambayo wanatibiwa bure lakini maeneo mengine bado wazee hawajapa huduma hiyo ya kutibiwa bure. Nafahamu Serikali yangu ni sikivu, itafanya utaratibu ili wazee hawa waweze kupata huduma bure na hasa walete sheria Bungeni ili iweze kufanyiwa utaratibu kusudi itambulike kihalali kabisa kwamba wazee wote sasa wanatakiwa kutibiwa bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, naomba niunge mkono hoja lakini nisisitize hospitali na vituo vya afya vile ambavyo havina waganga na wauguzi wapatiwe wataalam hao ili wananchi wetu waweze kupata huduma bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa naomba niunge mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Dkt. Kalemani, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishukuru Serikali ya CCM inayoongozwa na Jemedari Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu kwa kufanikisha mkopo wenye masharti nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Tumeahidiwa dola za kimarekani 140 sawa na shilingi bilioni 324,000.4 kwa ajili ya ya utekelezaji wa mradi muhimu sana wa maji Mto Malagarasi. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu utaweza kuwasaidia sana wananchi wa Mkoa wa Kigoma na mikoa jirani kwa sababu mradi wa umeme wa maji gharama zake ni ndogo kuliko za mafuta ambapo Mkoa wa Kigoma tumekuwa tukitumia generator kwa muda mrefu. Kupitia mradi huu ambapo tutakuwa tunatumia maji tutaweza kupata umeme wa uhakika na vilevile utakuwa ndio ukombozi wa wananchi wa Mkoa wa Kigoma na mikoa ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kuipongeza Serikali kwa miradi ya REA na kwa kutekeleza Ilani ya CCM kwa ahadi iliyotoa kwamba itaweza kuunganisha vijiji vyote kupitia miradi ya REA, naishukuru Serikali ya CCM. Sitaweza kuvitaja vijiji kwa sababu mimi ni Mbunge wa Mkoa nikianza kutaja vijiji vyote siwezi nikavimaliza, naomba vijiji vile ambavyo havijapatiwa umeme Serikali iweze kuwasimamia wakandarasi ili vijiji vile ambavyo havijapatiwa umeme viweze kupatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishauri Serikali kwa sababu kwa muda mrefu tumekuwa tukishauri kuhusu hifadhi ya mafuta ya dharura. Kwa kuwa na hifadhi hii nchi itaweza kufanya biashara na nchi zinazotuzunguka, kwa kuwa mafuta mengi yanayoingia nchini yanaenda nchi za nje. Kwa hiyo, nashauri Serikali iweze kuweka vivutio na kushauri wawekezaji wale wenye maghala waweze kujenga maghala mengine kusudi mafuta yawe yanahifadhiwa na hao wafanyabiashara na hatimaye mafuta yawe yanaweza kuuzwa nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, naomba Serikali itusaidie Mkoa wa Kigoma na hasa Wilaya ya Kasulu kwa sababu idadi ya watu imeongezeka na kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu mahitaji ya kupata umeme nayo yameongezeka. Naomba Serikali ipeleke nyaya za kutosha ili wananchi waweze kupatiwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naomba niunge mkono hoja. Nawapongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Naibu wake, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuhamasisha viwanda. Viwanda ni ajira, kwa sababu viwanda vikifanya kazi vitatumia malighafi inayotokana na wakulima kwa maana hiyo wanawake, vijana wataweza kupata kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili viwanda viweze kufanya kazi ni lazima malighafi nyingine itokane na kilimo. Kwa maana hiyo basi, nashauri kwa sababu viwanda vinahitaji malighafi kutoka katika sekta mbalimbali kwenye kilimo, uvuvi na mifugo, ni vizuri Serikali ikaweza kushirikiana ili sekta ya viwanda pamoja na kilimo vyote vikaenda kwa pamoja. Mfano, ili viwanda vya nguo viweze kufanya kazi ni lazima pamba ipatikane, wakulima waweze kulima pamba na pamba iweze kupelekwa viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye viwanda vya viatu tunapata mabegi, viatu, kwa hiyo, ngozi itatokana na wagufaji wa ng’ombe na kadhalika. Pia kwenye uvuvi tunapata viwanda vya samaki, kwa mfano, vile viwanda vilivyoko Mwanza vinatokana na uvuvi. Kwa maana hiyo, viwanda pamoja na sekta ya kilimo, ufugaji na uvuvi ni vitu ambavyo vinatakiwa viende sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika viwanda vya mafuta ni lazima tuwekeze kwenye kilimo cha mchikichi, alizeti na kadhalika. Katika ujenzi wa viwanda ni muhimu sekta ya kilimo nchini ikazingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanikisha mambo haya yote tukiwahamasisha wananchi wakaweza kulima kilimo cha mchikichi na Serikali ikawasaidia wananchi kuwapelekea pembejeo na miche naamini tutaweza kufanya vizuri katika zao hili na viwanda vya mafuta vitaweza kufanya kazi kutokana na malighafi tunayoizalisha sisi wenyewe kupitia kwa wakulima wetu. Kwa mfano, katika Mkoa wa Kigoma, naomba Serikali iwasaidie wananchi wa Kigoma kupata miche ya michikichi na pembejeo ili waweze kulima kilimo chenye tija katika zao la mchikichi na baadaye tuweze kupata viwanda vinavyoweza kutengeneza mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote niendelee kuomba Serikali iweze kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje kwenda kuwekeza viwanda Kigoma ili wananchi wakilima watapata sehemu ya kuuzia lakini pia ajira zitaweza kuongezeka. Naomba Serikali iweze kuongeza bajeti ya Wizara ya Biashara na Wizara ya Kilimo kufikia malengo tuliyojiwekea ya ujenzi wa viwanda. Bajeti ya Wizara ya Viwanda kwa kweli ni ndogo. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Viwanda na Biashara iweze kuongezewa bajeti ili iweze kufanya vizuri katika dhana ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna moja nililotaka kulizungumzia kuhusu OSHA. Naomba Serikali iandae mpango wa blue print ili tuweze kufanya vizuri katika nyanza hii kwa sababu malalamiko yamekuwa ni mengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu SDL wanayokatwa wafanyabiashara na wenye viwanda yote inapelekwa kwenye ujuzi. Naomba kiasi hiki kinachokatwa kiweze kurudishwa kipelekwe Wizara ya Viwanda na Biashara kwenda kuwasaidia watu wa SIDO na TIRDO ili kuongeza uwezo katika taasisi hizi. Kwa maana hiyo, naomba kabisa hayo yote niliyoyasema yaweze kuzingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii. Kwanza kabisa naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa kibali cha kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia hoja hii. Na mimi naomba niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Januari, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hiyo. Naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyoifanya katika Bwawa la Mwalimu Nyerere. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuweza kusimamia na kuweza kuiwezesha Wizara kuweza kufikia mahali walikofikia katika Bwawa la Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kuishukuru Serikali kwa ajili ya Mkoa wa Kigoma. Kwa muda mrefu Kigoma tulikuwa hatuko kwenye grid ya Taifa, lakini tangu mwaka jana umeme wa grid ya Taifa uliwashwa katika Wilaya nne na Wilaya tatu zilikuwa zimesalia, lakini niipongeze Serikali kwa Mradi wa Rusumo – Nyakanazi, kilovoti 400 zilizopatikana na ninaamini Wilaya zilizosalia kwa maana ya Kigoma Vijijini, Kigoma Mjini na Uvinza zitaweza kupatiwa umeme. Hivyo, ninaishukuru Serikali na ninaipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miradi ya REA wapo wakandarasi ambao wamefanya vizuri na wengine ambao hawajaweza kufanya vizuri. Na kwa sababu kwa mwaka huu Serikali iliahidi kwamba wananchi wote watakuwa wamepata umeme katika vijiji vyote, lakini bado umeme haujawafikia wananchi. Ninaomba Serikali iwasimamie wakandarasi wote wale ambao hawajaweza kukamilisha miradi hiyo ili waweze kukamilisha miradi hiyo kwa wakati na hatimaye vijiji vyote viweze kupatiwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Kigoma katika mradi wa umeme awamu ya kwanza hatukuwa tumepata umeme wa REA. Katika awamu ya pili hatukuwa tumepata umeme wa REA, lakini tumekuja kupata umeme wa REA katika awamu ya tatu. Tunamuomba Mheshimiwa Waziri asimamie wakandarasi hao ili umeme uweze kufika katika vijiji vingi lakini pia katika vitongoji. Kwa sababu ukiangalia maeneo mengi vijiji vichache ndivyo vimepata umeme na penyewe kwenye center, lakini vitongoji havijaweza kufikiwa na umeme. Tunaomba kwa sababu tumeshatoa ahadi kwa wananchi, wananchi wote wafikishiwe umeme hadi kwenye vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini zipo shule zetu za msingi na shule za sekondari nazo bado hazijapata umeme, vilevile na taasisi. Tunaomba Serikali ihakikishe umeme unawafikia wananchi, uwafikie wenye taasisi ili waweze kunufaika na umeme wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sana wapo wakandarasi ambao wengine wamefanya vizuri na wengine hawajafanya vizuri. Nirudie kusema kwamba Serikali iangalie wale ambao ni wababaishaji iwachukulie hatua na ikibidi wasiongezewe mikataba mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno hayo ninaunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, ili nami niweze kuchangia bajeti hii. Kwanza naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama jioni hii katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuunga hoja mkono bajeti hii ya Wizara ya Fedha na Mipango. Naomba nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, maarufu kama chambo kwa lugha la kiha, Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Katibu Mkuu Dotto, Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu nimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuweza kukubali kukutana na wafanyabiashara wanaotoka katika maeneo yote ya nchi ya Tanzania. Walikuwepo watu watano-watano kutoka katika wilaya, alikubali kupokea ushauri wao, akawaruhusu kutoa mawazo yao na akakubali kuwaruhusu kuweza kutoa kero zao. Kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Kigoma ambao ni wafanyabiashara na wanawake wote wa Tanzania ninamshukuru sana Rais kwa kuwaweza kutenga muda wake wa kukubali kukutana na wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kuishukuru sana Serikali kwa kuondoa tozo mbalimbali kwenye biashara mbalimbali, hatua hii itaendelea kuhamasisha wawekezaji kuweza kuendelea kuwekeza katika nchi yetu. Hii itasaidia sana kurudisha biashara maeneo mbalimbali ya nchi, ili wafanyabiashara waweze kufanya biashara yao bila kuwa na wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara nyingi zilifungwa kwa ajili ya kutokuwa na imani na watu wa TRA kutokana na wingi wa kodi na jinsi walivyokuwa wanatoza kodi kwa manyanyaso makubwa, lakini kwa hatua hii sasa wafanyabiashara wataweza kuwa na imani na Serikali yao na wataweza kufanya biashara kwa uhakika zaidi na bila usumbufu wowote. Kwa kweli, wafanyabiashara walienda kukata tama. Natokea Mkoa wa Kigoma, wengi walikuwa wanafunga biashara wanahangaika kukimbia huku na huku, ili labda waweze kutafuta sehemu ambayo hawawezi kupata manyanyaso, lakini kwa hatua hii nina amini na nina imani wafanyabiashara wataweza kuwa na hali ya utulivu na kuendelea kufanya shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba niungane na Wabunge wenzangu kama walivyosema na ninaomba nichangie katika maeneo matatu. La kwanza lilikuwa katika kodi, lakini la pili naomba kuzungumzia viwanda na malighafi inayotakiwa kutumika viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa viwanda kama vile walivyosema Waheshimiwa Wabunge wenzangu ni lazima kuhakikisha tunahamasisha matumizi ya malighafi zinazotokana na na mazao ya kilimo kama vile mchikichi, kahawa, pamba, tumbaku, chai, korosho, n.k. Tukijenga viwanda vya namna hii wananchi wetu wataweza kupata soko na uhakika wa soko kwa hiyo, wataweza kuzalisha kwa wingi kwa sababu watakuwa sasa wanajua wakizalisha watapeleka bidhaa zao wapi, lakini ajira itapatikana kutokana na viwanda vitakavyokuwa vimejengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kama ifuatavyo kwa mfano, katika Mkoa wa Kigoma lipo zao la mchikichi. Mkoa wa Kigoma lipo zao la mchikichi ambalo zao hilo linapatikana katika Mkoa wa Kigoma na viwanda vinavyotumia mahitaji ya zao la mchikichi vitazalisha bidhaa kama vile mafuta, sabuni, mashudu kwa ajili ya chakula cha mifugo, n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bidhaa ya mafuta, sabuni na mashudu zitatumika kwa ajili ya Wananchi wa Kigoma na Wananchi wa Tanzania, kwa ujumla. Kwa hiyo, tukizalisha kwa wingi hatutaweza tena kutumia pesa zetu za kigeni kwenda kununua bidhaa nje, tutaweza kununua bidhaa zetu za ndani ya nchi. Kwa hiyo, nilikuwa ninaiomba Serikali kwa vile sasa Kigoma inaanza kuzalisha mchikichi na kwa sababu sasa hivi wananchi wameshakuwa tayari sasa kuweza kuanza kulima kilimo cha mchikichi, ninaiomba Serikali iweze kusaidia mbegu, ili wananchi waweze kulima kilimo chenye tija. Kwa sasa mbegu ni tatizo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niunge mkono hoja iliyotolewa. Hakuna mtu anayepinga mambo ya Wizara. Wizara ilitoa maelekezo kwamba wafanyabiashara watafute leseni, watafute TIN number ili waweze kufanya biashara zao vizuri. Elimu hiyo haijawafikia watu wengi. Kwa hiyo watu wanahangaika, wanatupigia simu kila mara, utaratibu upi ufanyike?

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kabisa tangu Mheshimiwa Bashe akiwa back bencher alikuwa ni mtetezi wa wakulima. Tunamwomba ajipambanue ili wakulima waweze kuuza mazao yao maeneo mbalimbali wanakotaka. Kwa sababu mpaka sasa hivi wakulima walikuwa tayari wamepata wateja kutoka maeneo mbalimbali katika mikoa mbalimbali. Kwa mfano, sisi Kigoma tuko mpakani walikuwa wanapata wateja kutoka Tabora, Musoma, Kagera na wengine kutoka Uganda. Tunaiomba Serikali iweze kutoa tamko, wakulima waendelee kuuza mazao katika sehemu mbalimbali. Hivyo basi, tunafahamu Mheshimiwa Bashe ni mkulima na anawapenda wakulima…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, tunaomba atoe mchanganuo ili wakulima waweze kunufaika kwa kuuza mazao yao nje. Ahsante. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuzungumza jioni hii ya leo. Kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwenye wingi wa rehema kwa kunijalia afya na kunipa kibali cha kuweza kusimama ndani ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba niunge mkono hoja ya hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. Ili kukuza uchumi pamoja na sekta ya uzalishaji ni lazima tuimarishe miundombinu ya barabara pamoja na nishati ya umeme. Tunamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Magufuli tumeshuhudia ndani ya utawala wake barabara zimejengwa na zinaendelea kujengwa, reli ya SGR inajengwa, bwawa la Nyerere katika Mto Rufiji linajengwa, hizi zote ni juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna imani miradi hii yote ikikamilika nchi yetu itaendelea kupaa, wananchi wataweza kuanzisha viwanda vikubwa na vidogo hivyo wataweza kusafirisha mazao yao katika maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa sababu usafiri utakuwa ni wa uhakika, lakini pia tutakuwa tumeweza kupata umeme wa uhakika. Kwa maana hiyo wataweza kukuza kipato chao na kuchangia pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kuhusu kilimo, kilimo kimeajiri watu wengi sana takribani zaidi ya watu asilimia 58 ni wakulima wakiwemo wanawake. Hivyo basi, naomba niishauri Serikali, bajeti ya kilimo iongezwe kusudi iweze kufanya vizuri katika kilimo. Ninyi wote ni mashahidi, mchana tulienda nyumbani kupumzika lakini tulirudi tukiwa tumepata chakula, chakula kinachotokana na kilimo. Kwa hiyo, naomba niwashawishi Waheshimiwa Wabunge, tuhakikishe bajeti ya kilimo inaongezwa ili wananchi wetu ambao wengi wamejiajiri kwenye kilimo waweze kunufaika kupitia kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti ikiongezeka tutaweza kupata pembejeo na dhana bora za kilimo, lakini kilimo cha umwagiliaji kitaweza kufanyika vizuri kwa sababu miundombinu itakuwepo. Kwa mfano katika Mkoa wetu wa Kigoma, tunalo bonde la Mto Lwiche, bonde nzuri sana, ambalo tunaweza kulima kilimo cha umwagiliaji tukalima kilimo cha mpunga, kikaweza kuwanufaisha wananchi kwa chakula, lakini pia wakizalisha mchele wanaweza kuuza hata nje ya nchi wakaweza kuongeza kipato chao na kuweza kuchangia pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu zao la mchikichi; tunaishukuru sana Serikali kwa kulifanya zao la mchikichi kuwa zao la kimkakati, Serikali imeweza kutoa miche ya mbegu lakini bado haitoshelezi kwa sababu wananchi wameitikia kilimo hicho. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iendelee kutusaidia kuongeza miche ili wananchi waweze kuzalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu zao la mchikichi pamoja na alizeti vikiweza kulimwa na kutoa matunda, tutaepukana kuagiza mafuta kutoka nje ya nchi kwa sababu pesa nyingi tumekuwa tukizutumia kwenda kununua mafuta nje ya nchi, lakini tukizalisha sisi wenyewe tutaweza kunufaika kupitia kilimo chetu cha ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba kuchangia kuhusu ushirika, katika ushirika bado hatujafanya vizuri kwa sababu wananchi kwanza hawana elimu, lakini hata Maafisa Ushirika wenyewe bado ni wachache. Kwa hiyo, elimu inayotolewa kwa Vyama vya Ushirika, SACCOS na SACCAS bado haitoshelezi, kwa hiyo, naomba niishauri Serikali iweze kuongeza juhudi za kutoa elimu katika Vyama vya Ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimalizie kwa kuwashukuru wanawake wa Mkoa wa Kigoma, walionichagua kwa kura nyingi, walifanya ya kwao lakini wakanichagua nikaweza kurudi ndani ya Bunge lako Tukufu, kwangu mimi Wajumbe wale ni wema kwangu sana. Nawashukuru sana lakini nakishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuweza kuniteua na kugombea hatimaye nikaibuka mshindi. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa na nzuri iliyokwishafanya kufikisha maji vijijini. Kazi imeshaanza na inaendelea na mwenye macho haambiwi tazama maana kazi kubwa inaendelea kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumejaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji, ikiwa ni pamoja na maziwa, mito mikubwa pamoja na mito midogo midogo. Kwa kutumia fursa hizo nashauri tutumie vyanzo hivyo tulivyojaliwa na Mwenyezi Mungu kuhakikisha tunafikisha maji vijijini. Maji ni uhai, maji ni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wengi vijijini wamejiajiri katika shughuli za kilimo. Hivyo basi, maji yakifikishwa vijijini watapata nafasi ya kwenda kushughulika na shughuli nyingine za kuzalisha mali na kuchangia kipato chao na pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishindwa kufikisha maji vijijini wananchi wengi wakiwemo wanawake wataweza kupata magonjwa ya matumbo na tutaweza kutumia pesa nyingi kwa ajili ya kununulia dawa. Tukifikisha maji vijijini tutaweza kuepusha magonjwa na pesa zitaweza kwenda kufanya shughuli zingine badala ya kwenda kununua dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri kuhusu kilimo cha umwagiliaji. Kwa kutumia vyanzo hivyo hivyo vya maji tuendelee kuimarisha kilimo cha umwagiliaji. Ipo miradi ya maji ambayo ilianzishwa, tunaomba miradi hiyo iendelezwe na iweze kukamilika na mingine mipya iweze kuanzishwa ili kwa kutumia maji tuliyojaliwa na Mwenyezi Mungu tuweze kunufaika kwa kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, wananchi wengi wamehamasika kulima michikichi na wamehasika haswa na imepelekea wananchi wengi kulima kilimo hiki. Naiomba Serikali iendelee kutusaidia mbegu. Kwa awamu ya kwanza tumeshapata mbegu za kutosha, tunaomba sasa Serikali iendelee kuongeza mbegu ili wananchi wale ambao tayari wameshahamasika waweze kulima kilimo cha michikichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kila anapopata nafasi anafika Kigoma. Tunakushukuru sana kwa kuweza kuuangalia Mkoa wa Kigoma na kuweza kufanya zao la mchikichi liwe zao mkakati. Kwa juhudi ambazo umeendelea kutuonesha na sisi tutaendelea kukuunga mkono kuhamasisha wananchi waendelee kulima zao hilo la mchikichi hatimaye tuweze kupata mazao ya mchikichi tuachane na kuagiza mafuta nje, tuweze kutumia mafuta tunayozalisha wenyewe. Pesa za kigeni tunazotumia kuagiza mafuta nje zibakie kwetu na kuweza kufanya shughuli nyingine za maendeleo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kuweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuunga mkono hoja hii na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Aweso na Naibu wake pamoja na wafanyakazi wa Wizara ya Maji kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya.

Mheshimiwa Spika, maji ni uhai, maji ni kila kitu. Sisi Tanzania tumejaaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji; bahari, maziwa, mito mikubwa na midogo, lakini kwa kiasi kikubwa maji haya hayajaweza kuwafikia wananchi. Kwa hiyo, naomba kutokana na bahati tuliyopata Watanzania kwa kupata vyanzo hivyo, basi viweze kumaliza tatizo la maji vijijini. Tusitumie kuchimba visima tu, lakini pale ambapo ipo mito mikubwa, maji yatolewe kwenye ile mito mikubwa yapelekwe kwenda kusambazwa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna Mto Malagarasi una maji mengi sana. Tulikuwa tunaomba kupitia mto huo, vijiji vile ambavyo vimekaribiana na mto huo viweze kunufaika kwa kupitia maji yanayotoka katika Mto Malagarasi. Vile vile zipo Halmashauri ambazo zinayo miradi ilianzishwa kwa muda mrefu, lakini haijaweza kukamilika. Naiomba Serikali iweze kupeleka pesa ili ile miradi ambayo tayari ilishaanzishwa kwa muda mrefu iweze kukamilika na wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanawake wengi wanatumia muda mwingi kwenda kutafuta maji na wanashindwa kufanya shughuli za kuzalisha mali. Kwa hiyo, wananchi wakipatiwa maji, wanawake wataweza kutumia muda mwingi kwenda kuzalisha mali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Sp[ika, vile vile ukosefu wa maji unasababisha milipuko ya magonjwa mengi ikiwemo kipindupindu na kuhara, kama wenzangu walivyosema, fedha nyingi zinaenda kutumika kwa ajili ya ununuzi wa madawa. Pia naomba shule za msingi na sekondari zipelekewe maji. Zipo shule nyingine hazina maji kabisa. Watoto wanapata shida na hasa watoto wa kike, wanapata shida kutokana na maumbile yao. Mtoto wa kike anatakiwa kupata maji kila wakati. Kwa hiyo, naomba maji yapelekwe shuleni; katika shule za msingi na sekondari ili watoto waweze kuondokana na adha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia karibia kila mwezi Watoto wa kike, wapo ambao wanapoteza siku tano hawaendi shuleni kabisa kutokana na maumbile yao, wanashindwa kwenda shule. Matokeo yake, zile siku tano ambazo mtoto anakuwa hakwenda shule, anapoteza muda wa kusoma, hawezi kufanya shughuli zake za masomo vizuri. Sasa siku tano hizo za kila mwezi, ukizidisha kwa mwaka mzima, mtoto wa kike amepoteza siku ngapi? Ni siku nyingi kabisa. Matokeo yake baadhi ya watoto wanaathirika na kutokufanya vizuri kwa sababu ya ukosefu wa maji mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Kasulu una tatizo kubwa la maji, iwe kiangazi iwe masika, mji ule maji yanayotoka ni machafu. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali itusaidie kututengenezea kichujio ili maji yanayotoka katika Mji ule yaweze kuwa masafi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika eneo la Mwandiga nalo bado kuna shida ya maji. Mabomba yametandikwa, miundombinu imesambazwa lakini bado maji hayajafika katika Mji wa Mwandiga; na Mji huo kwa muda mrefu sana, wanapata shida ya maji. Kwa hiyo, naomba kwa sababu miundombinu imeshasambazwa, mabomba yaweze kuletwa kusudi maji yaweze kupatikana katika Mji wa Mwandiga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika katika Mji wa Kibondo tulipatiwa shilingi milioni 700, lakini bado maji hayajawafikia wananchi. Nilikuwa naomba basi, Serikali iweze kupeleka fedha hizo haraka iwezekanavyo ili kuweza kukamilisha miundombinu hiyo wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu na ninaomba nianze kwa kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Engineer Masauni pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu kwa jinsi anavyoendelea kuwapigania Watanzania wa rika zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila nikimwangalia Mheshimiwa Dkt. Mwigulu pamoja na Mama Samia ninakumbuka mbali sana. Mwaka 2015 wakati wakitafuta kura walikuwa wanatembea Pamoja; mama na mtoto wote walikuwa wakiruka kwa chopa kuhakikisha Serikali ya CCM inashinda. Sasa ninaiangalia bajeti yao ya kwanza Mheshimiwa Mama Samia akiwa Rais wa Awamu ya Sita jinsi gani wanavyofanya kazi mama na mtoto, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Mama Samia kwa namna alivyoshusha pressure ya wafanyabiashara kwa kuwahamasisha kulipa kodi bila shuruti. Namshukuru sana Mheshimiwa Mama Samia na wananchi wamelipokea kwa furaha kubwa sana na pressure zao zimeshuka kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uwezeshaji wa wanawake na vijana. Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Halmashauri zetu imehamasisha wanawake na vijana kuwezeshwa ili waweze kujiajiri hatimaye waweze kupata kipato na kuchangia kodi katika Taifa letu pale watakapokuwa wameweza kusimama vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee kuhusu wanawake wafanyabiashara wa Kariakoo. Soko la Kariakoo la vitenge limekamatwa na wanawake. Wanawake hawa walihangaika kutafuta mitaji, hatimaye wakasimama na wakaweza kuagiza mizigo kutoka nchi za nje na wamekuwa wakifanya vizuri na wamekuwa wakilipa kodi vizuri sana, lakini kutokana na kodi kutokuwa Rafiki, wamefika mahali wanashindwa kufanya biashara zao kwa sababu kodi inakuwa hailipiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sisi tumezungukwa na nchi za DRC, Zambia, Uganda na nchi zote ambazo zimetuzunguka zimekuwa zikija kuchukua biashara Tanzania, lakini baada ya kuwa kodi siyo rafiki kwa wafanyabiashara wa Tanzania wale wote waliokuwa wakija Tanzania kununua vitenge wamehamia nchi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za nyuma walikuwa wakilipa kodi 0.4 na wakati huo walipokuwa wakilipa namna hiyo walikuwa wanaweza kuchangia kwa mwezi shilingi bilioni 9.7 mpaka shilingi bilioni 10. Kwa maana hiyo, wafanyabiashara wa Kariakoo kila mwezi walikuwa na uwezo wa kushusha makontena kuanzia 90 mpaka 120; na kontena moja limekuwa likilipwa kwa shilingi milioni 128. Nchi jirani ya Zambia kontena hilo ambalo Tanzania wanalipa shilingi milioni 128 wao wanalipa shilingi milioni 30. Angalia tofauti iliyopo, ni karibia shilingi milioni 100 nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kugundua hivyo, nchi jirani zilizotuzunguka wameteka masoko ya Watanzania, wanaagiza biashara wao wenyewe na biashara zile zinapita kwenye bandari ya Tanzania. Wanapitisha nchini mwetu, wanazipeleka nchini kwao, baadaye zinarudi nchini mwetu kwa sababu vitenge vilivyopo Tanzania, vya kwetu sisi havina…(Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki anachokizungumza mzungumzaji, kwanza nimpongeze kwa sababu ni kweli kwamba soko la vitenge la Kariakoo limeingia mchanga. Kwa sababu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maua ambayo yanatengenezwa kwenye vitenge vya Tanzania ndiyo yanaongoza kwa ubora katika East Africa na Afrika nzima, lakini kutokana na kupanda kwa kodi kutoka 0.4 na kwenda kwenye 0.6 tumepoteza kabisa soko kwa Watanzania wengi, wamekuwa stranded. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Kenya, Uganda, Zambia… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sanga usichangie. Karibu Mheshimiwa Genzabuke, malizia.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake. Kwa maana hiyo, wapo wafanyabiashara ambao tayari wameshahama Tanzania wameenda kuwekeza nchi za nje, lakini wanawake wameshindwa kuhama kwa sababu mama ni mlezi. Mama hawezi kuhama akamwacha baba, mama hawezi akahama akawaacha watoto. Kwa hiyo, wale wameshindwa kuhama wamebaki hapa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kilio hiki kimfikie Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mpendwa, Mama Samia Suluhu aangalie jinsi ya kuwasaidia wanawake hawa ambao ni walipa kodi wazuri, wamekuwa wakiipigania Tanzania ili biashara hii iendelee kubaki Tanzania, Tanzania iendelee kupata kodi kupitia wafanyabiashara wa Tanzania kuliko nchi jirani kuendelea kunufaika na bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara zinapita kwenye bandari yetu zinaenda nchi za Jirani, baadaye zinarudi Tanzania. Tanzania inakuwa haiingizi mapato, mapato yanapotea, hatupati wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nami niweze kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mpenzi Mama Samia Suluhu kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya watanzania. Lakini nimpongeze sana kwa kuweza kutuletea chanjo ya UVIKO-19 na kututoa woga tukaweza kuchanja. Mwenyewe tayari nimeshachanja mwanzo nilikuwa na wasiwasi, lakini sasa hivi nimechanja, lakini na wewe nakushukuru kwa kutuhamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kuwashukuru vilevile wasaidizi wake; Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dkt. Mpango, Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya wanapita huku na kule kwenda kuwahamasisha watanzania na kuangalia shughuli zinazofanywa nchi nzima nawapongeza sana na Mawaziri pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa fedha nyingi ambazo amepeleka Tanzania nzima fedha kwa ajili ya barabara kila Jimbo, fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya na fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa madarasa. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sasa madarasa yanajengwa na nyumba za walimu nazo ziweze kujengwa na niipongeze Serikali kwa kuwa tayari ilishaanza kuajiri walimu, iendelee kuajiri walimu ili madarasa yanapojengwa, nyumba za walimu zinapopatikana na walimu vilevile waweze kuwa wengi na waweze kufanyakazi ya kufundisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natokea maeneo ya wakulima na wapiga kura wangu ni wakulima ukiangalia wakulima wengi wamejiajiri kwenye kilimo wakiwemo wanawake na vijana. Nilikuwa naomba Serikali iongeze bajeti kwa ajili ya kilimo, kwa mfano; ukiangalia mwaka tumekumbana na changamoto ya mbolea kupanda na kufikia mfuko mmoja shilingi 120,000. Ninaomba tuweze kuita wawekezaji waweze kujenga viwanda hatimaye mbolea iweze kushuka bei na wakulima wetu waweze kulima kilimo chenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusu umeme; ipo mikoa ambayo haijaunganishwa kwenye grid ya Taifa, Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Rukwa. Nilikuwa naomba mikoa hiyo iweze kupewa kipaumbele na yenyewe iweze kuunganishwa kwenye grid ya Taifa, kwa sababu ukiwaunganisha kwenye grid ya Taifa mikoa hiyo wawekezaji wataweza kwenda kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano; Mheshimiwa Waziri Mkuu kila siku unakuja Kigoma kuja kuhamasisha kilimo cha mchikichi, lakini kama hakutakuwepo na umeme wa grid ya Taifa wananchi wakizalisha michikichi watakosa kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba kwa heshima na unyenyekevu mkubwa kabisa umeme wa grid ya Taifa uweze kufika kwenye mikoa hiyo minne niliyoitaja ikiwemo na Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari upo mradi ambao ulishaanza kuanzia Tabora, Uvinza mradi huo unaendelea naomba Serikali iongeze pesa ili mradi huo uweze kukamilika. Mheshimiwa Makamu wa Rais alipokuja mwezi wa nane alielekeza mradi huo uweze kukamilika Oktoba 2021. Kwa hiyo, naiomba Serikali katika Mpango tunao upanga sasa ipeleke pesa kusudi umeme wa grid ya Taifa uweze kufika Kigoma hatimaye wawekezaji waje kuwekeza Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu hata hospitali zitaweze kunufaika kwa sababu kwa sasa hivi si wa uhakika hatuwezi kuwa na vifaa kama MRI, ST-Scan. X-Ray na Ultra Sound umeme wa uhakika ukiwepo vifaa hivyo vitakuja na wananchi wataweza kurahisishiwa maisha kwa sababu sasa hivi wanafuata matibabu wengine wanaenda Mwanza, wengine wanaenda Dar es Salaam na kutokana na kipato chao kidogo wengine wanapoteza maisha. Kwa hiyo naendelea kuomba umeme wa grid ya Taifa uletwe Kigoma na maeneo mengine mikoa ile ambayo sikuweza kuitaja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu, naendelea kuishukuru Serikali ya CCM katika Mkoa wetu wa Kigoma ujenzi wa barabara wa kilometa 260 wa kutoka Nyakanazi – Kibondo – Kasulu mpaka Buhigwe unaendelea. Tunaomba pesa zipelekwe ili barabara hiyo iweze kukamilika barabara ambayo inaunganisha mikoa, lakini vilevile inatuunganisha na nchi za jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwenye sura ya pili kuhusu hali ya uchumi; nikupongeze wewe mwenyewe kwa sababu kwanza umeendelea kuwaelimisha wananchi na kutuelimisha sisi Wabunge kwa kusema kwamba zipo sheria ambazo wakati mwingine zinahitajika kurudi Bungeni ili zifanyiwe marekebisho kusudi ziweze kuwasaidia watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari yetu ya Dar es Salaam inapitisha mizigo mingi sana, mizigo hiyo inapita inaenda nchi za jirani na mizigo hiyo inarudishwa tena kuja kuuzwa ndani ya nchi yetu. Nilikuwa ninaomba Mheshimiwa Waziri aangalie kipengele hicho ambacho kitawasaidia wazawa waweze kufanya biashara katika nchi yao. Tofauti na sasa hivi mizigo inapitishwa nchini mwetu inaenda nchi za jirani halafu inakuja kuuzwa nchini kwetu. Kwa hiyo, wazawa hawawezi kushindana na wale ambao wamepitisha mizigo nchini kwetu wanaenda kuuza kwa bei ya chini halafu sisi tunauza kwa bei ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushukuru sana, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa Rehema kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu ili kuchangia hoja ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kuunga mkono hoja ya Waziri Mkuu kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niipongeze Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inayoongozwa na Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na viongozi wote waliopo Serikalini kwa jinsi wanavyofanya kazi na kupita maeneo mbalimbali wakihamasisha shughuli za maendeleo. Nitakuwa mwizi wa fadhila nisipoishukuru Serikali ya CCM. Unapopata kidogo ni lazima ushukuru. Ninaishukuru sana Serikali ya CCM kwa kuweza kuendelea kuufungua Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Kabingo – Kibondo mpaka Buhigwe yenye urefu wa kilometa 260 inaendelea kujengwa. Sasa, niiombe tu Serikali iongeze fedha ili barabara hiyo ikamilike mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze mama yetu mpendwa kwa kutupatia fedha ya COVID-19 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa nchi nzima na kila jimbo; tunamshukuru sana mama yetu. Mwaka huu hakuna mtoto ambaye amemaliza form IV na anatakiwa kwenda shuleni ambaye amebakia nyumbani, wote wameweza kwenda shule. Wapo wengine ambao walisafiri kwenda maeneo mbalimbali kabla ya matokeo kutoka. Niwaomba wazazi wao wawahamasishe watoto hao ili waende shule kusoma kwa sababu nafasi zipo na madarasa yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwaombe viongozi wa elimu waliopo kwenye majimbo na Wilaya zetu, kuhakikisha watoto wote waliochaguliwa kwenda Sekondari waweze kwenda Sekondari. Nisiishie hapo, niendelee kuipongeza Serikali kwani zahanati, vituo vya afya pamoja na hospitali za Wilaya zimejengwa na nyingine zimekarabatiwa; kwakweli tunamshukuru sana Mama yetu mpenzi kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia katika maeneo mawili. Eneo la kwanza ni kuhusu nishati ya umeme na eneo la pili ni kuhusu kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo mikoa ambayo bado haijaunganishwa kwenye grid ya taifa, mikoa hiyo ipo minne, ambayo ni; Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Katavi pamoja na Rukwa. Niiombe, kwasababu mikoa hiyo ipo pembezoni, Serikali ifanye kila namna kusudi mikoa hiyo nayo iweze kufaidi matunda ya taifa kwa kuunganishwa kwenye grid ya taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Kigoma zipo njia mbili. Njia ya kwanza ni grid ya taifa kutoka Tabora kuja Kigoma kwa KV 132. Ninaomba, mradi huu ambao tayari umeanzishwa ukamilike, kwasababu mpaka sasa hivi mradi ule unasuasua. Kwa hiyo, nilikuwa ninaomba TANESCO waongezewe bajeti ili iweze kukamilisha mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo pia mradi wa kutoka Nyakanazi – Kigoma nao tena unatakiwa kukamilika kwasababu mwanzo Serikali walisema kwamba ungeweza kukamilika 2022. Kwa hiyo tunaomba juhudi ziongezeke ili miradi hiyo ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme ukishapatikana Mkoa wa Kigoma utafunguka. Hii ni kwasababu Mkoa wa Kigoma ni lango kuu la uchumi, ni Mkoa ambao umepakana na nchi za DRC, Burudi na hata wakati mwingine Zambia. Kwa hiyo basi umeme ukishapatikana wawekezaji watakuja kujenga viwanda Kigoma, na kwasababu watu wa nchi hizo zinazotuzunguka wanachukua bidhaa kutoka Kigoma; kwa hiyo hawatakwenda mbali, watachukulia bidhaa kutoka katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma tuna Bonde la Lwiche. Kama umeme ukipatikana tunaweza kufanya kilimo cha umwagiliaji; kusaidia juhudi za Serikali za kuhamasisha kilimo; kwasababu tutaweza kusukuma mitambo ya kumwagilia mashamba yetu kwasababu umeme utakuwa wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kuweka mpango wa kuhakikisha mbolea ipatikane kwa bei rahisi, kama mbolea ikipatikana kwa bei rahisi wananchi wetu wataweza kuzalisha kwa wingi zaidi wakiwemo na wanawake. Mimi ni mama, ninawakilisha wanawake. Ni kwamba, wanawake wa taifa hili ni wazalishaji wakubwa, ni wakulima wazuri sana. Kwahiyo, wakipata mbolea wataweza kuzalisha kwa wingi, watapata chakula na kuongeza kipato kutokana na uzalishaji wa mazao watakayokuwa wamelima.

Mheshimiwa Mwenyekiti,niendelee kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu amefanya kazi kubwa ya kuhamasisha kilimo cha Mchikichi Mkoani Kigoma, tunamshukuru sana, kazi aliyoifanya inaanza kuonekana, michikichi baadhi inaanza kutoa matunda. Kwa hiyo tunaomba Serikali iendelee kutuangalia Mkoa wa Kigoma katika zao letu la Michikichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wameweza kuendelea kuelewa maana ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: …Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: …naunga Mkono hoja (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja hizi mbili. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa rehema kunijalia afya na kunipa kibali cha kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali namna inavyofanya kazi. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Januari Makamba, Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya. Wasichoke waendelee kuwa wabunifu na kuendelea kulitumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafsu hii kumponeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu kipenzi Samia Suluhu Hassan kwa namna alivyoandika historia Tarehe 22/12/2022 kwa uzinduzi wa ujazaji maji katika Bwawa la Mwalimu Nyerere. Nampongeza sana Mama kwa kazi nzuri aliyoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza kwenye maeneo mawili. Eneo la kwanza, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuandika historia kwa mara ya kwanza mwaka jana kuweza kuwasha umeme wa Gridi ya Taifa katika Mkoa wetu wa Kigoma. Nashukuru sana Mungu aendelee kuibariki Serikali yetu inayoongozwa na Mama yetu mpendwa kwa kuweza kuukumbuka Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Kigoma wakiwemo wanawake tunatoa shukrani nyingi sana kwa kuweza kutuunganisha kwenye Gridi ya Taifa. Mkoa wetu una Wilaya Sita, Wilaya zilizokwisha pata umeme huo ni Wilaya ya Kakonko Kibondo, Kasulu na Buhigwe. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri Januari Wilaya zile ambazo bado hazijapata neema ya kupata umeme huo, kwa maana ya Wilaya ya Kigoma Vijijini, Kigoma Mjini na Uvinza nazo ziweze kunufaika kwa kupatiwa umeme pindi itakapowezekana, kwa sababu tukipata umeme watu wa Kigoma tutaweza kuzalisha na kuweza kuwahamasisha wawekezaji waje kuwekeza katika Mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu tayari umefunguka kwa sababu barabara zinaendelea kujengwa na tukipata umeme tutaweza kukimbia sawasawa na wenzetu ambavyo wamekuwa wakikimbia. Kwa mara ya kwanza umeme ule ulipokuja changamoto kidogo huwa hazikosi, ulikuwa unakatika katika lakini kwa sasa kutokana na jinsi Serikali inavyoendelea kuimarisha miundombinu nafikiri tutaenda vizuri tutaondokana na kukatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya miradi ya umeme, miradi yake inatekelezwa kwa kusuasua nilikuwa ninaomba sasa, Serikali ijitahidi kuhakikisha miradi inakamilika. Kwa mfano, mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, mradi wa Rusumo na mradi wa Kinyerezi. Miradi hiyo ikikamilika itatusaidia sana kwa sababu umeme utakuwa ni wa uhakika na ninyi mnafahamu kabisa umeme ukikatika katika hatuwezi kufanya shughuli za uzalishaji kwa maana hiyo basi umeme huo wa miradi hiyo mikubwa ukikamilika utaweza kutusaidia kuondokana na tatizo la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Bwawa la Mwalimu Nyerere lingekuwa limeshakamilika sasa kwa vile mmeongezewa muda mjitahidi kuhakikisha mradi huo unakamilika mara moja. Pia, nilikuwa ninashauri upande wa REA, baadhi ya miradi ya REA imeshindwa kukamilika kwa wakati hali inayosababisha vijiji vingi kukosa umeme, kumekuwa na malalamiko wakati mwingine kwamba kuna ukosefu wa vifaa kwa ajili ya kuunganishia umeme, naomba Serikali ijitahidi kuwasimamia wale Wakandarasi ambao walichukua kazi maeneo mbalimbali ili waweze kukamilisha kazi kwa wakati na kuweza kuwaondolea wananchi wetu adha ya ukosefu wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba niendelee kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya, ninaamini mkifanya kwa kudhamiria tutaweza kuondokana na tatizo la umeme. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa rehema kwa kunijali afya na kunipa kibali cha kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba niunge mkono hoja. Napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM, nampongeza sana Rais wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kusahau ninaomba nimwombe Mheshimiwa Waziri; kwanza nimpongeze kwa kuajiri walimu na watumishi wa afya. Baada ya hapo niombe ombi maalum, naomba watumishi waalimu na wa kada ya afya waletwe Mkoa wa Kigoma, Kigoma ya sasa si ya zamani. Sasa hivi tuna barabara na zinaendelea kujengwa, lakini pia tumeshapata umeme wa grid ya Taifa; kwa hiyo Kigoma ni maeneo mazuri ya kuweza kuishi watumishi kwa sasa. kwa hiyo tunaomba mtuletee watumishi, Kigoma sasa hivi tuna barabara na tuna umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapongeza kwa jinsi vituo vya vilivyojengwa zahanati, hospitali za wilaya, vilevile hospitali za mikoa zikakarabatiwa na nyingine zikapatiwa hadhi ya kuwa hospitali za rufaa, ikiwemo na Hospitali ya Mkoa wetu wa Kigoma. Ombi maalum; ninaomba mtuletee watumishi. Kwa mfano katika Wilaya ya Kasulu tumeweza kupatiwa fedha bilioni 3.6, kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu, lakini tulipata msaada kutoka kwa wadau milioni 500 kwa ujenzi wa nyumba za watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nyumba tunazo na miundombinu ni mizuri. Tumepata vifaa vya thamani ya bilioni 1.5 kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Kasulu DC ambayo ni Hospitali mpya ya Wilaya ya Halmashauri ya Kasulu DC. Hivyo basi changamoto tuliyonayo ni kwamba hatuna watumishi, hatuna wataalamu wa mionzi, maabara na huduma ya meno. Kwa hiyo tunaomba tupatiwe wataalam angalau hata watano kuja katika Halmashauri ya Kasulu DC kwa sababu hospitali hiyo ni mpya inahitaji wataalam wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ombi moja; Kata ya Kagera Nkanga ipo kilometa 80 kutoka Makao Makuu ya wilaya; ninaomba tujengewe kituo cha afya kwa sababu ni kutoka kituo hicho kuja mjini kilometa 80 tunaweza kuangalia ni kwa umbali gani. Wanawake wanapoteza maisha kwa ukosefu wa huduma ikiwemo kupoteza damu nyingi wanapokuwa wamecheleweshwa kufikishwa kwenye hospitali ya wilaya. Si hivyo tu, eneo hilo kuna majambazi wanateka sana katika aneo hilo la kutoka Kagera Nkanda kuja Kasulu au Kasulu kwenda Kagera Nkanda, kilometa 80. Angalia, kilometa zote hizo kwenda kufata huduma eneo lingine tunaomba kituo cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Buhigwe, wilaya anayotoka Makamu wa Rais, na wakati alipokuwa akigombea, alienda katika Kata ya Mkatabnga akashuhudia wananchi wametumia nguvu wameshaanza kujenga jengo la kituo cha afya. Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Angellah Kairuki nakuomba sana, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa wananchi wameshajitolea wameshaweka msingi wana matofali ya akiba, nakuomba mama yangu utupatie kituo cha afya katika Kata ya Mkatanga Kijiji cha Kitambuka. Nakuomba sana utusaidie kwa sababu wananchi wameshaonesha njia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa Mheshimiwa Waziri ninaomba uiangalie TARURA kwa macho ya huruma kwa sababu, kwa mfano sisi Mkoa wa Kigoma hatuna mgodi wa dhahabu, wananchi wetu ni wakulima na kilimo kinafanyika shambani. Tunaomba utupatie pesa ili barabara zinazoenda mashambani barabara zinazounganisha vijiji na vijiji, barabara zinazosafirisha mbolea kupeleka mashambani ziweze kujengwa kwa mfuko wa TARURA. Kwa hiyo tunaomba TARURA waongezewe pesa barabara zinazoenda mashambani zinazounganisha vijiji vyetu ziweze kujengwa na kupitika kiurahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno hayo nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwenye wingi wa rehema, kwa kunipa kibali cha kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, naunga mkono hoja. Nami niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuamua kwa moyo wake wa dhati kufanya kilimo cha Tanzania kiwe cha kuwaletea wananchi chakula, kilimo cha kuleta ajira vilevile kiwe ni kilimo cha kibiashara, nampongeza sana Rais wangu. Pia nampongeza Makamu wa Rais, Dkt. Mpango, kwa uhamasishaji wa zao la mchikichi. Naomba nimpongeze Mheshimiwa Bashe Waziri wa Kilomo, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Kilimo, hongera sana kwa kazi mnayoifanya. Nitakuwa sijatenda haki nisipompongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu nitajielekeza katika maeneo mawili. Eneo la kwanza ni mchikichi, eneo la pili nitazungumzia mbolea. Kwa nini nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, tangu mwaka 2018 Serikali ilipoamua mchikichi kuwa zao la kimkakati Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa akija Mkoani Kigoma kuhamasisha kilimo cha zao la mchikichi na wananchi walihamasika wanaendelea kuhamasika na kwa sasa ni miaka mitano michikichi ile aliyokuwa akiihamasha na mchikichi alioupanda yeye mwenyewe katika eneo la JKT Bulombora tayari umeishaanza kuzaa matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Bashe, Naibu wako ameshafika Kigoma, ninakuomba ukimaliza Bunge hili uje ujionee maajabu yanayofanyika Mkoa wa Kigoma katika zao la mchikichi. Gereza la Kwitanga wanafanya vizuri sana, wana mashamba makubwa sana ambayo tangu kilimo cha mchikichi kilipoanza kuhamasishwa wameweza kulima. JKT Bulombora wana mashamba makubwa sana na wanaanza kuzalisha michikichi kuwagawia wananchi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Bashe tunakuomba ufike Kigoma.

Mheshimiwa Spika, wananchi wamehamasika, wamelima, bado kuna changamoto kwenye miche ya michikichi, mahitaji bado ni makubwa. Lakini niishukuru Serikali kwa kutenga ruzuku kwa ajili ya miche ya michikichi. Ninakuomba sasa Mheshimiwa Bashe ufike Kigoma.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Benki ya TIB. Wananchi wamekuwa wakihamasishwa kwenda kuomba mkopo TIB, lakini ni ukweli usiofichika kwamba masharti bado ni magumu. Ninaiomba Serikali kupitia Waziri wa Ardhi, waweze kupimiwa mashamba yao ili waweze kupata hati miliki, mashamba yao yaweze kuwadhamini, hatimaye waweze kukopesheka, bila hivyo bado masharti ni magumu. Kwa hiyo, ninaomba Serikali ihamasishe, Waziri wa Ardhi, wananchi wapimiwe mashamba yao wapate hati miliki ili waweze kukopesheka kupitia hati miliki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuzungumzia kuhusu mbolea. Ninamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuwapatia wananchi mbolea. Tuliipata mbolea ambayo wananchi wameweza kupata kwa shilingi 70,000. Kwa kweli tunashukuru, kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Kigoma ninamshukuru sana Mama kuweza kutupatia mbolea ya ruzuku. Bado kuna changamoto.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Bashe nikushukuru kwanza, yalipokuwa yakitokea matatizo madogo madogo wakati wa ugawaji wa mbolea kila tulipokupigia simu ulipokea simu na ulitoa maelekezo na watendaji wako waliweza kufanya kama ulivyowaelekeza.

Mheshimiwa Spika, mwanzoni mbolea zilikuwa zinapelekwa Makao Makuu ya Wilaya. Ninakuomba sasa Mheshimiwa Bashe, mbolea ziende kwenye Tarafa na kila Kata ili kila mwananchi atakapohitaji mbolea iwe karibu yake. Kwa sababu wananchi wamepata mateso sana kwa ajili ya ufuatiliaji wa mbolea kutoka vijijini kuja Makao Makuu waliweza kupata shida sana, walilazimika kulala mjini siku mbili, tatu, wakipanga foleni kusubiri mbolea, pia walilipia nyumba za wageni ili waweze kujihifadhi wakati wanasubiri mbolea. Naomba marekebisho yafayike ili waweze kunufaika kwa kupata mbolea bila kupata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vipo vifungashio, mara nyingi mbolea inafungwa kwenye mifuko ya kilo 50 na kilo 25. Wale wakulima wadogowadogo na hasa akina mama wengine ambao hawana uwezo wa kununua mfuko wa kilo 50 au kilo 25, naomba uhamasishe iweze kuwepo mifuko inayofungasha kilo 20, kilo 15, kilo 10, kilo tano hadi kilo mbili ili mbolea iweze kuwafikia hata wananchi wa kipato cha chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimuombe Waziri, yapo malalamiko ya mawakala waliofanya kazi ya kusambaza mbolea zaidi ya miaka mitano na wamekaa kwa matumaini kwamba ipo siku watalipwa pesa zao, Mheshimiwa Waziri nataka nikuulize; je, watu hao watalipwa pesa hizo wanazozidai? Kama hawatalipwa waambieni ukweli waache kusubiri wakati uwezekano wa kulipwa pesa hizo haupo! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno hayo nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu Mwenye wingi wa Rehema kwa kunipa kibali cha kusimama ndani ya Bunge lako tukufu. Namshukuru sana Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu kwa jinsi inavyowatumikia Watanzania. Nampongeza Mheshimiwa Bashe kwa kazi nzuri anayoifanya, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wote tunafahamu kwamba Sekta ya Kilimo imeajiri watu wengi sana. Asilimia 65 ya Watanzania wote wameajiriwa na kilimo, wakiwemo wanawake na vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imejipanga kwa ajili ya kukiinua kilimo. Kilimo kikipewa kipaumbele wananchi wataweza kufanya vizuri katika kilimo. Ni ukweli usiopingika kwamba wananchi wakiwekewa mazingira wezeshi katika kilimo wataweza kufanya vizuri. Naomba sasa Mheshimiwa Waziri, Serikali iweze kutoa ruzuku kwa ajili ya mbolea. Kwa muda mrefu sana mbolea imekuwa ikileta shida kwa wakulima. Maeneo mengine mbolea inachelewa kufika na tunafahamu kabisa kwamba mvua za kwanza ni zakupandia na maeneo yanatofautiana. Kigoma na Rukwa ni tofauti, na hata Tanga. Kwa hiyo, mvua zinazoanza kunyesha Kigoma pengine Tanga zinakuwa hazijanyesha. Kwa hiyo, tunaomba mbolea ifikishwe kwenye maeneo husika mapema kabla wakulima hawajaanza kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuishukuru Serikali kwamba kwa muda mrefu tumeona imekuwa ikitumia pesa nyingi kuagiza mafuta kutoka nje, lakini kwa sasa Serikali imedhamiria kabisa kuhakikisha mazao yanayotoa mafuta yanapewa kipaumbele. Naishukuru Serikali kwa kuendelea kutusaidia sisi watu wa Kigoma, na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi anavyoendelea kuhamasisha michikichi katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkoa wa Kigoma walihamasishwa na wakahamasika kulima kilimo cha mchikichiki. Walio wengi tayari wamelima michikichi na inaanza kutoa matunda. Hata hivyo, bado mahitaji ya miche ya michikichi ni makubwa sana. Kwa hiyo, naiomba Serikali iendelee kutusaidia miche ya michikichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunipatia miche 3,000. Mheshimiwa Waziri naomba uendelee kuniongeza miche mingine kwa sababu mimi ni mama ninayezunguka Mkoa mzima wa Kigoma na mahitaji ya miche ya michikichi ni ya Mkoa mzima. Kwa hiyo, naomba niongezewe miche mingine ya michikichi ili wananchi waweze kulima kilimo hiki na hasa wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile zao la alizeti nalo wananchi wameweza kuitikia kulima zao hilo. Naomba katika mikoa ile ambayo itapewa mbegu ya alizeti naomba na Kigoma nayo iweze kupewa kwa sababu alizeti inastawi katika Mkoa wetu wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, kwa sasa mazao katika Mkoa wetu wa Kigoma mahindi na maharage kwa wakati huu wanapovuna bei ipo juu kidogo. Niendelee kumwomba Mheshimiwa Waziri mipaka iwe wazi ili wananchi waweze kuuza mazao yao nje ya nchi, kwa sababu wakiuza mazao yao nje ya nchi wanapata bei ambayo ni nzuri. Kwa hiyo, wanaweza kunufaika wao wenyewe, lakini wanarudisha gharama wanazozitumia wakati ule wanapokuwa wanalima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzunguma maneno hayo, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)