Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Freeman Aikaeli Mbowe (8 total)

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kumuuliza Waziri Mkuu swali.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, wewe ukiwa kama Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni na wewe ukiwa kama mwanasiasa mzoefu, nina hakika unatambua kwamba ujenzi wa demokrasia ni gharama na ni mchakato wa muda mrefu. Nina hakika utakuwa utajua vilevile kwamba nchi yetu imepiga hatua kubwa katika kujenga jamii inayoheshimu demokrasia, inayoheshimu Sheria na inayoheshimu Katiba ya nchi. Katika muda mfupi tangu Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani, yapo mambo matano makubwa yaliyotokea ambayo yanaashiria, aidha Serikali hiyo haiheshimu kukua kwa demokrasia katika Taifa ama pengine ina dhamira ya kuondoa lengo kubwa hilo lililowekwa na Katiba ya Taifa.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, mambo hayo ni pamoja na baada tu ya uchaguzi wa mwaka 2015, Jeshi la Polisi limeweka makatazo nchi nzima kwa Vyama vya Siasa kufanya kutokufanya kazi zake za kisiasa, haki ambayo ni haki ya kikatiba.
Leo tayari ni miezi mitatu na siku tatu katazo hilo linaendelea na katazo hilo Mheshimiwa Waziri Mkuu uliliunga mkono na kulisisitiza katika mkutano wako uliofanywa katika Jimbo lako la Ruangwa, kwamba wenye haki ya kufanya ni wale walioshinda, lakini Vyama vya Siasa haviendelei kuruhusiwa kufanya kazi hiyo ya siasa. (Makofi)
Swali langu sehemu (a) ni kama ifuatavyo; Mheshimiwa Waziri Mkuu unataka kuithibitishia Bunge hili, nchi hii na dunia hii, kwamba wewe kama Kiongozi Mkuu wa Serikali una kusudio la kuendelea kuzuia Vyama vya Siasa kufanya kazi zake za kisiasa ambayo ni haki yao ya Kikatiba? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Swali la pili, Mheshimiwa Waziri Mkuu, tukiendelea hapo hapo unatambua vilevile kwamba urushaji wa matangazo ya moja kwa moja ni haki ya Kikatiba ya wananchi kupata taarifa na Shirika la Habari la Taifa ni shirika la umma, lakini ndani ya Bunge kuna taarifa zilizo rasmi kabisa kwamba Serikali yako imetoa kauli hapa kuzuia urushaji huo wa matangazo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sambamba na uzuiaji wa urushaji huo wa matangazo kumeendelea kuwepo matumizi makubwa ya majeshi yetu kuanzia Zanzibar hadi hapa na Zanzibar katika kupinga matokeo ya uchaguzi wa Zanzibar ambao ulikuwa ni uamuzi wa wananchi?
Mheshimiwa Waziri Mkuu unaiambia nini dunia kwamba Awamu yako ya Tano sasa imekubali kuwa na utawala wa kijeshi kwa mgongo wa utawala wa kidemokrasia? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme namshukuru sana Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwa maswali yake mawili ambayo yanahitaji ufafanuzi na Watanzania waweze kujua, kwamba uongozi huu wa Awamu ya Tano ni uongozi ambao unaongoza kwa kufuata demokrasia, kanuni, sheria na taratibu kadri ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, yapo mambo yanajitokeza na tunapojaribu kutoa maelekezo ya kimsingi ya kuweza kufuatilia na kwa sababu ya utaratibu wa mazoea tu yanaweza kutafasiriwa vinginevyo. Suala lako la makatazo ya Vyama vya Siasa kufanya mikutano, ni jambo ambalo naweza kusema msemaji wa kwanza kabisa hakutumia nafasi yake ya uandishi kuandika kwa mfululizo kwa sababu ni mimi ndiye ambaye nilikuwa nimefanya ziara kwenye Jimbo langu kusalimia wapiga kura wangu.
Mimi ni Mbunge kama nyie na ninapokuwa Ruangwa sivai koti la Waziri Mkuu bali nakuwa Mbunge nazungumza na watu wangu. Nimekuwa na vikao mbalimbali vya makundi mbalimbali nikiwashukuru binafsi kwenye Jimbo langu ambako najua tuna utamaduni wetu. Nimepita pia kwenye Kata ambazo pia Madiwani wetu ni wa Vyama vya Upinzani, lakini tumeweka msimamo wa vyama vyote katika Jimbo lile kwamba lazima sasa tufanye kazi za maendeleo kwenye Jimbo letu.
Mheshimiwa Spika, kama mwandishi yule angeweza kuweka mtiririko wa ziara zangu na matamko yetu ndani ya Wilaya yangu kwa Jimbo langu, angeweza kunitendea haki, kwa sababu nilichotamka mimi kilifuatiwa na kauli zilizotamkwa na Madiwani kwenye Kata ambako nimetembela wakiwemo wa upinzani, ambao walisisitiza na kutoa msimamo kwamba sasa Jimbo hili tunataka tufanye kazi suala la siasa tunaliweka pembeni na tunaondoa tofauti zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, haya yanazungumzwa na Madiwani wenzangu wa vyama vingine. Kwa hiyo, ni jambo jema wanapolitamka kwa wananchi kwa maana ya kuweka msimamo wa maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mtiririko ule tulizungumza pia na Baraza la Madiwani, nimezungumza na wafanyakazi wa Halmshauri, nimezungumza na Baraza la Wazee, nimezungumza na akinamama na pia nikazungumza na Jeshi la Polisi, wale ni sehemu ya raia walioko kwenye Jimbo langu. Mimi nimefanya kazi nyingi kwao na wao wamefanya kazi nyingi sana kwangu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kauli yangu ilikuwa inatokana na mazingira yale, kama mwandishi angeamua kufanya kazi yake vizuri kwa kueleza shughuli zangu hata nilipotamka kwamba kuanzia sasa sisi tumeamua tufanye kazi, bila kuzingatia itikadi za vyama vyetu na kwamba sasa mambo ya siasa tuache pembeni. Wale wote ambao sasa wangetakiwa kupita kwenye maeneo ya walioshinda ni wale tu ambao wameshinda kwenye maeneo yao. Kwa hiyo jambo lile kama lingekuwa limeelezwa, limeripotiwa kwa mtiririko ule wala lisingeweza kuleta tafsiri ambayo imekuja kutolewa.
Mheshimiwa Spika, najua utawala wa sheria, najua Vyama vya Siasa vina haki yake, najua nchi inatambua kwamba chama cha siasa kinaweza kufanya mkutano. Pia kama msingi ule wa kauli ya Wanajimbo wa Ruangwa unaweza kufuatwa na watu wengine unaweza kuwaletea tija pia.
Mheshimiwa Spika, kwa hayo niliyosema, niseme tu kwamba, jambo lile lilitokana na mazingira ninamoishi na sikulitamka kama Waziri Mkuu, nilitamka kama Mbunge wa Jimbo na lilitokana na matamko ya sisi wawakilishi wa Vyama vya Siasa kutoka kwenye Jimbo lile Mheshimiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni lile ambalo Mheshimiwa ametaka kujua suala la kauli ya Serikali juu ya TBC kuacha kutangaza siku nzima na badala yake watatangaza vipindi vya maswali na majibu, lakini baada ya hapo wataendelea na shughuli zao na huku waki-record ili waweze kututangazia baadaye.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amelifafanua vizuri sana jana kwenye kipindi maalum na naamini Watanzania wametuelewa. TBC haijaacha kutangaza, walichofanya ni kubadilisha ratiba. Matangazo ya Bunge yataendelea kutangazwa, lakini tumebadilisha muda, badala ya muda ule ambao wao wangeweza kufanya matangazo ya kibiashara na matangazo mengine, suala la Bunge waandishi wao wako, TBC ina wawakilishi Dodoma, watafanya recording, halafu baadaye watatafuta muda mzuri ambao pia tunaamini Watanzania wengi watapata muda mzuri wa kuweza kuyasikiliza matangazo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, huo ni mpango wa Taasisi yenyewe wa ndani, unaotokana na kazi wanazozifanya, wanajua matatizo na faida wanazozipata ndani ya Taasisi. Kwa hiyo, wanapoishauri Wizara, wanapoieleza Wizara na kwa kuwa walishaanza kutekeleza na Watanzania waliona mkatiko wa matangazo, lakini pia kulikuwa na mwongozo ulitolewa hapa. Kwa hiyo, tukasema jambo hili ni lazima sasa tulieleze kesho yaani lazima kuwe na kauli ya Serikali kwa Watanzania kwa sababu Mwongozo ulitolewa na mmoja kati ya Wabunge wetu anataka kujua kwa nini kuna mkatiko wa matangazo. Kwa hiyo, ndivyo ilivyokuwa na huo nadhani ni msimamo wa TBC na ndiyo msimamo wa Serikali.
SPIKA: Tunaendelea na Mheshimiwa Kiongozi wa Upinzani swali la nyongeza!
MBUNGE FULANI: La majeshi bado.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa ametaka pia kujua matumizi ya Majeshi. Majeshi yetu yapo kwa malengo kwamba lengo kuu ni kutunza amani na utulivu ndani ya nchi. Wajibu wao mkubwa ni kuhakikisha kwamba watu kwa maana ya Watanzania kwa Majeshi ya Tanzania, wajibu wake ni kuhakikisha kwamba watu wetu wanafanya shughuli zao kwa amani na utulivu na wako nchi nzima. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jukumu lao ni kumlinda Mtanzania popote alipo bila ya kukiuka misingi ya jambo ambalo anatakiwa kulifanya wakati huo. Wapo Zanzibar, wapo pia Tanzania Bara na wote hao kazi yao na jukumu lao ni lilelile. Sasa wanaweza kulazimika kutumia nguvu pale ambapo wanaona utaratibu uliowekwa eneo hilo unakiukwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo kazi ya Jeshi la Polisi, kwamba wataendelea kutunza amani ili Watanzania waliokuwa kwenye eneo hilo kila mmoja afanye shughuli yake. Kila mahali kuna utaratibu wake na kila mahali kuna msingi wake na tunatarajia katika eneo, wote walio kwenye hapo, wanaofanya jambo hilo, wafanye jambo hilo kwa msingi unaofanana, usiokiuka taratibu za eneo hilo.
Kwa hiyo, Jeshi la Polisi lipo na litaendelea kufanya kazi yake kwa uaminifu, kwa uadilifu na naomba sana tuwasaidie Jeshi la Polisi kufanya kaziWAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa ametaka pia kujua matumizi ya Majeshi. Majeshi yetu yapo kwa malengo kwamba lengo kuu ni kutunza amani na utulivu ndani ya nchi. Wajibu wao mkubwa ni kuhakikisha kwamba watu kwa maana ya Watanzania kwa Majeshi ya Tanzania, wajibu wake ni kuhakikisha kwamba watu wetu wanafanya shughuli zao kwa amani na utulivu na wako nchi nzima. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jukumu lao ni kumlinda Mtanzania popote alipo bila ya kukiuka misingi ya jambo ambalo anatakiwa kulifanya wakati huo. Wapo Zanzibar, wapo pia Tanzania Bara na wote hao kazi yao na jukumu lao ni lilelile. Sasa wanaweza kulazimika kutumia nguvu pale ambapo wanaona utaratibu uliowekwa eneo hilo unakiukwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo kazi ya Jeshi la Polisi, kwamba wataendelea kutunza amani ili Watanzania waliokuwa kwenye eneo hilo kila mmoja afanye shughuli yake. Kila mahali kuna utaratibu wake na kila mahali kuna msingi wake na tunatarajia katika eneo, wote walio kwenye hapo, wanaofanya jambo hilo, wafanye jambo hilo kwa msingi unaofanana, usiokiuka taratibu za eneo hilo.
Kwa hiyo, Jeshi la Polisi lipo na litaendelea kufanya kazi yake kwa uaminifu, kwa uadilifu na naomba sana tuwasaidie Jeshi la Polisi kufanya kazi yao bila ya usumbufu ili wasionekane wanafanya kazi nje ya utaratibu wao. Hilo ndiyo jibu la msingi. (Makofi)
MHE. FREEMAN A. MBOWE:
Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu maswali.
Mheshimiwa Waziri Mkuu unatambua kwamba sasa hivi nchi ina uhaba mkubwa wa sukari. uhaba huu wa sukari umesababishwa na amri iliyotolewa na Mheshimiwa Rais mwezi Februari mwaka huu ya kuzuia uagizaji wa sukari bila kufuata utaratibu ama kufanya utafiti wa kutosha kuhusiana na tatizo zima ama biashara nzima ya uagizaji na usambazaji wa sukari katika Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunatambua kwamba nchi yetu inazalisha takribani wastani wa tani milioni 300 na zaidi ya tani 180 hivi zinaagizwa kutoka nchi za nje na sasa hivi wewe mwenyewe umetoa kauli kwamba Serikali imeagiza sukari.
Sasa swali langu ni hili; maadam sukari ina utaratibu maalum wa uagizaji ambao unasimamiwa na Sheria ya Sukari ya mwaka nafikiri Sugar Industry Act ya mwaka 2001 na kwamba Bodi ya Sukari inatoa utaratibu maalum wa uagizaji wa sukari hii na biashara ya uagizaji sukari sio tu uagizaji kwa sababu ya fedha ni pamoja na muda maalum, circle maalum wakati gani agizo hili isingane na uzalishaji katika viwanda vya ndani ambavyo Mheshimiwa Rais alidai alikuwa na
nia ya kuvilinda ambalo ni jambo jema.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, sasa unaweza ukatuambia hiyo sukari uliyoagiza umeiagiza kwa utaratibu gani? Anaiagiza nani? Inategemewa kufika lini? Ni kiasi gani? Na itakapofika haitagongana na uzalishaji katika viwanda vyetu local baada ya kuisha kwa msimu wa mvua na hivyo kusababisha tatizo la sukari kwa mwaka mzima ujao?
WAZIRI MKUU:
Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbowe, Mbunge wa Hai na Kiongozi wetu wa Kambi ya Upinzani kwa kuuliza swali hili kwa sababu tulitaka tutumie nafasi hii kuwaondoa mashaka Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wakati wote anapotoa tamko ni kutokana na mwelekeo na mpango wa Serikali ambao umepangwa kwa lengo maalum. Sukari nchini ni k
weli kwamba inaratibiwa na Bodi ya Sukari ambayo pia imewekwa kisheria na moja kati ya majukumu yao kufanya utafiti, lakini pia kusimamia viwanda vinavyozalisha kwa lengo la kusambaza sukari nchini na iweze kutosha.
Mheshimwia Spika, kwa miaka mitatu, minne ya nyuma, sukari imekuwa ikiletwa kwa utaratibu ambao baadaye tuligundua kwamba unavuruga mwenendo wa viwanda vya ndani na viwanda vya ndani havipati tija. Kwa hiyo, Serikali hii ilipoingia madarakani moja kati ya mikakati yake ni kuhahakikisha kwamba viwanda vya ndani vinalindwa, unavilindaje? Ni pale ambako sasa sukari inayoingia ndani lazima idhibitiwe lakini pia kuhamasisha viwanda hivyo kuzalisha zaidi sukari. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mahitaji ya sukari nchini ni tani 420,000. Sukari ambayo inazalishwa nchini ni tani 320,000 na upungufu ni kama 100,000 hivi. Tani 100,000 hii kama hatuwezi kuiagiza kwa utaratibu na udhibiti mzuri kunaweza kuingia kwa sukari nyingi sana kwa sababu kwenye sukari tuna sukari za aina mbili, sukari ya mezani ile ambayo tunaitumia kwenye chai na sukari ya viwandani na haina utofauti mkubwa sana kwa kuingalia na sukari ya viwandani na ya
mezani ni rahisi sana kwa mwagizaji kama hatuwezi kudhibiti vizuri unaweza kuleta sukari nyingi ya mezani halafu kukajaa sokoni.Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kauli ya Mheshimiwa Rais ni katika mpango wa kulinda viwanda vya ndani kama ambavyo umekiri, lakini jukumu la Bodi sasa ya Sukari baada ya kauli ile inatakiwa sasa iratibu vizuri. Kwa hiyo, sukari imeratibiwa vizuri na bodi ya sukari na mahitaji ya sukari ile ya tani 100,000 na
mahitaji ya sukari ambayo inatakiwa kuingia ili isivuruge uzalishaji ujao ni kazi ambayo inafanywa Bodi ya Sukari.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza ya kumuuliza Waziri Mkuu swali.
Mheshimiwa Spika, kwa hali ilivyo nchini sasa hivi kiuchumi, kuna mdororo mkubwa wa uchumi, na katika mdororo huu wa uchumi ambao tuna imani kabisa katika hatua za baadaye utaathiri bajeti ya Serikali, wawekezaji wengi wanasita kuwekeza katika nchi kwa sababu ya kutokuwa na uhakika kuwa Tanzania ya kesho itakuwaje. Kuna kuporomoka sana kwa deposits ama amana zinazowekwa katika benki zetu za biashara, mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam, mizigo katika Bandari ya Tanga, mizigo katika border posts za Namanga, Sirari, Horohoro na Tunduma imepungua kwa zaidi ya asilimia 60.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, baadhi ya makampuni ya usafirishaji kwa zaidi ya asilimia 40 yamefunga kazi zao au vyombo vyao vya usafirishaji, kwa maana ya malori makubwa yamesitisha safari na makampuni mengine yamehamia nchi nyingine za jirani kwa sababu ya kutokuwa na uhakika wa hali ya ndani.
Je, hali hiyo kama Serikali mnaijua? Na kama mnaijua mnachukua hatua gani za makusudi za kurekebisha hasa ikizingatiwa kwamba uchumi unapoporomoka, kama ilivyo Tanzania leo mazao ya wakulima kama mbaazi, nafaka, mpunga nao unaanguka bei na tayari umeshaanguka bei kwa kiwango kikubwa?
Mheshimiwa Waziri Mkuu, mna mkakati gani wa makusudi wa kurekebisha hali hii? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nianze leo kwa kujibu swali la Mheshimiwa Mbowe, Mbunge na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwa swali lake muhimu kwa sababu linagusa hali ya uchumi ndani ya nchi.
Mheshimiwa Spika, tunapozungumia hali ya uchumi tunazingatia mambo mengi na nikiri kwamba maeneo yote uliyoyatamka ni sehemu kubwa ya mchango wa hali ya uchumi nchini. Na kwa kutambua kwamba uchumi unashuka, inabidi tufanye tathmini ya kutosha, ingawa maeneo uliyoyatamka kwamba yamepungua sana nayo pia kuna haja ya kujiridhisha na kupata takwimu sahihi za miaka iliyopita na hali tuliyonayo sasa ili tujue kama je, kiwango cha kushuka kimesababishwa na nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali haitaweza kulala, malengo ya Serikali wakati wote ni kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi unaongezeka. Moja ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kwamba uchumi unakua kupitia nyanja zote pamoja na maeneo uliyoyatamka. (Makofi)
Kwa hiyo, kupungua kwa mizigo bandarini kumekuwa kunazungumzwa na watu wengi na juzi juzi Kamati yetu ya Bunge ya Viwanda na Biashara ilikuwa bandarani kupitia hayo na wamekaa na wadau. Lakini wadau peke yao hawatoshi, ni lazima tupate pia taarifa kutoka ndani ya Serikali na mwenendo wa uendeshaji wa bandari, mipaka yetu, lakini pia mazao yetu ndani ya nchi na mwenendo wake mzima. (Makofi)
Kwa hiyo, niseme kwa sasa kukupa takwimu halisi za kuporomoka au kutoporomoka si rahisi sana, lakini nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwamba Serikali itafanya jitihada wakati wote kuhakikisha kwamba uchumi wake unapanda. Serikali itakubali kukutana na wadau kuzungumzia hatma ya uchumi nchini, Serikali itapokea ushauri kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge kwa namna ambavyo wanaona kwamba kuna udhaifu mahali ili tuweze kuhakikisha kwamba uchumi unaongezeka na pia bajeti ya mwakani inapata mafanikio makubwa ukilinganisha na bajeti ambayo tunaitekeleza sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi bado nirudie kukuhakikishia kwamba Serikali haitalala katika hili kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi unapanda na kwa hiyo, kama changamoto ya maeneo ambayo umeyatamka tutafanya mawasiliano na Wizara ya Fedha lakini pia na Benki Kuu ili tuweze kupata takwimu halisi za hali ya uchumi nchini na tutakuja kulijulisha Bunge letu ili Wabunge wajue na wapate nafasi ya kutushauri. Kamati yetu ya Kudumu ya Biashara na Viwanda ipo, bado ina nafasi nzuri ya kuweza kutushauri kama Serikali. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona lakini nilisikitika kwamba unadai hujaniona, lakini nashukuru umeniona hatimaye. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali la msingi la kisera.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni siku ambayo Taifa letu linaadhimisha siku ya Haki Duniani. Tunapoadhimisha siku hii ya Haki Duniani ambayo nina hakika leo Spika wetu yupo Dar es Salaam kwa ajili ya jukumu hilo akiungana na viongozi wengine wa Kitaifa akiwemo Mheshimiwa Rais na Jaji Mkuu. Ni miezi mitatu kamili tangu Mheshimiwa Godbless Lema, Mbunge wa Arusha akamatwe nje ya geti la Bunge na kupelekwa kizuizini kushtakiwa kwa kesi inayoitwa ya uchochezi ambayo ina dhamana, lakini miezi mitatu leo hajaweza kupata dhamana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tuna Mbunge mwingine wa Kilombero, Mheshimiwa Lijualikali ambaye anatumikia kifungo cha miezi sita katika Gereza la Ukonga kule Dar es Salaam na kazi ngumu; wakati huo huo, tuna zaidi ya Madiwani sita wa Chama cha CHADEMA ambao wamefungwa kwa makosa yenye misingi ya kisiasa; tuna viongozi kama Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa wa Lindi aliyefungwa miezi nane kwa kufanya kazi yake ya kisiasa. Tuna viongozi wa ngazi mbalimbali zaidi ya 215 aidha wamefungwa ama wanaendelea na mashtaka mbalimbali katika maeneo mbalimbali ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona namna Serikali inavyotumiwa mawakala na vibaraka wake kukigawa na kukidhoofisha Chama cha Wananchi (CUF) ikiwemo kumtumia Msajili wa Vyama vya Siasa kudhoofisha Upinzani. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, maadam Mheshimiwa Rais alishatangaza kwamba kusudio lake ni kufuta vyama vya upinzani kabla ya mwaka 2020, haya yanayoendelea katika Awamu ya Tano ambacho ni kinyume na utamaduni na mazoea yetu kama Taifa, ni sera au utekelezaji wa sera hiyo ya kuua upinzani; na ni sera chini ya Serikali yako na Mheshimiwa Magufuli?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nikanushe kwamba Mheshimiwa Rais hajawahi kutangaza kuvifuta Vyama Vya Upinzani.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Spika umesema kwamba Watanzania wote wanajua kwamba nchi hii inaongozwa kwa sheria, kanuni na taratibu, lakini pia tunajua katika kuendesha nchi tunaendesha kwa mihimili mitatu. Iko Serikali, Mahakama na Bunge. Hakuna mhimili unaoweza kuingilia mhimili mwingine. (Makofi)
Tatu, Watanzania wote wanajua kwamba jambo lolote ambalo liko Mahakamani haliwezi kuzungumzwa mahali pengine popote. Kwa hiyo, siwezi kutumia nafasi hii kuzungumzia mambo yote yaliyoendelea chini ya sheria na yaliyoko Mahakamani. Ahsante sana.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Mheshimiwa Waziri Mkuu nafikiri una hakiki kutokana na vyanzo vyako mbalimbali kwamba Taifa katika wakati huu linakumbwa na sintofahamu, hofu na taharuki nyingi zinazosababishwa mambo kadhaa.
Mheshimiwa Spika, moja na la msingi ambalo napenda kukuuliza ni kwamba kuna hofu kuhusu haki ya kikatiba ya kuishi na kupata hifadhi. Kuna hofu kuhusu haki ya kikatiba ya kupata na kutoa habari ambayo inaweza kuchagizwa kwa kiwango kikubwa na kukosekana kitu kama
uhuru wa Bunge kusikika kwa wananchi ambao wametutuma mahali hapa.
Mheshimiwa Spika, kuna hofu kuhusu watu kupotea, watu kutekwa na jambo hili limetawala sana kwenye mijadala katika mitandao na vyombo vya habari na mfano halisi ukiwemo kupotea kwa msaidizi wangu Ben Saanane ni miezi sita sasa Serikali haijawahi kutoa kauli yoyote, haielezi ni nini kinafanyika jambo ambalo linapelekea pengine kuamini aidha, Serikali haitaki kufanya uchunguzi ama imeshindwa kufanya uchunguzi. Mheshimiwa Waziri Mkuu unalipa Taifa kauli gani kuhusu hofu na taharuki hii ambayo imelikamata Taifa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia kwamba Taifa lina hofu ya kikatiba kwenye maeneo kadhaa lakini pia amerejea michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge iliyokuwa inazungumzia suala la usalama wa nchi kwamba Taifa na Watanzania wana hofu na kwamba bado Serikali hatujatoa kauli.
Mheshimiwa Spika, kupitia majibu yangu lakini pia wakati wa bajeti yangu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, jambo hili mara lilipojitokeza tulitoa taarifa ya awali na mimi niliwasihi Watanzania kwamba Taifa letu kwanza ni Taifa ambalo kwa miaka mingi limekuwa na utamaduni mzuri wa watu kuheshimiana, watu kufuata misingi, kanuni, sheria na taratibu. Pia tunatambua kuwa kumetokea matukio mbalimbali kwa miaka mingi huko na matukio haya tumeendelea kuyaachia vyombo vya usalama kufanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa jambo ambalo limejadiliwa sana na Waheshimiwa Wabunge na hofu ambayo imekuwa ikielezwa kwamba Watanzania wana hofu, nilitumia nafasi yangu kuwasihi Watanzania kwanza waiamini Serikali yao kwamba moja kati ya majukumu ya Serikali yetu ni kuhakikisha Watanzania wanaishi kwa amani na kwa uhakika wa ulinzi wa wao wenyewe na mali zao wakati wote. Pia hata Serikali yetu nayo imeweka azma hiyo na kwamba jambo hili tunaendelea kuliimarisha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kupitia michango hiyo pia hata Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi alieleza na mimi nikarejea kuimarisha hili kwamba Watanzania tunaomba mtupe muda, vyombo vyetu vinaendelea kufanya kazi ya kuchunguza ili tuweze kubaini ni nini hasa sasa kinatokea na ni kwa nini Watanzania wanafikia hapo kuwa na hofu. Haya yote huwezi kutoa matamko hadharani zaidi ya kuwasihi Watanzania kuwa watulivu na kutoa ushirikiano kwa Taifa na kwamba vyombo vyetu vinapofanya kazi kama tutaweza kueleza haraka maazimio yetu tunaweza tukapoteza njia nzuri ya kupata vyanzo vya kwa nini kasoro hizi zinajitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nirudie tena na nimsihi sana Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwamba Serikali ipo na imesikia haya kutoka kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge. Naomba niwasihi tena Watanzania kuwa na imani na Serikali yenu kwamba tunaendelea na ufuatiliaji wa matukio yote yaliyozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge tuone kwa nini yanajitokeza, nani anasababisha kwa sababu vyanzo vya matatizo haya ni vingi na vinahitaji uchunguzi wa kina ili tuweze kujua hasa dosari iko wapi na tuweze kudhibiti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wito wangu kwa Watanzania, tuendelee na utamaduni wa kutoa taarifa kwa vyombo vyetu pindi tunapojua kwamba hapa kuna jambo au linaandaliwa au limetokea na aliyesababisha ni fulani ili tuweze kuchukua hatua za papo kwa papo ili tuweze kunusuru watu wengine wasiweze kukubwa na matukio hayo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge mwenzangu na Kiongozi mwenzangu hapa Bungeni tuendelee kuipa muda Serikali kufanya ufuatiliaji wa jambo hili na baadaye tutakapogundua kabisa tutakuja kuwapa taarifa ili Watanzania wawe na uhakika na shughuli zao wanazoendelea nazo. Ahsante sana.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza ya kumuuliza Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Bunge kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 63(2), ndicho chombo kikuu chenye mamlaka na wajibu wa kuisimamia na kuishauri Serikali. Katika Bunge hili, Bunge la Kumi na Mabunge mengine kadhaa, Bunge limekuwa linatoa Maazimio kadhaa kuitaka Serikali itoe taarifa na Serikali imekuwa inaahidi kutoa taarifa, lakini taarifa nyingi ambazo ni Maazimio ya Bunge yamekuwa hayatekelezwi na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna Maazimio ya Bunge kuhusiana na Tokomeza mpaka leo Serikali haijaleta majibu. Kuna Maazimio ya Bunge kuhusiana na ESCROW na IPTL, Serikali mpaka leo haijatoa majibu. Kuna Maazimio ya Bunge kuhusu mabilioni ya Uswis, Serikali mpaka leo haijatoa majibu na Maazimio mengine mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri Mkuu unaliambia nini Bunge na unaliambia nini Taifa. Wewe kama Kiongozi wa Serikali Bungeni, utapenda kusema kwamba Serikali inalidharau Bunge ama Serikali haina majibu ya kutoa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe, Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nikuhakikishie kwamba Serikali inaheshimu sana Mhimili wa Bunge na inathamini sana maamuzi ya Mhimili huu wa Bunge na tutaendelea kushirikiana na Mhimili wa Bunge katika kupata ushauri na namna nzuri ya kuendesha Serikali kwa mapendekezo ambayo yanatolewa na Waheshimiwa Wabunge kupitia chombo cha Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua vikao kadhaa huko awali kumekuwa na Maazimio yanayoitaka Serikali ilete maelezo, lakini baadhi ya maeneo ambayo yanatakiwa kuletwa hapa ni yale ambayo yanahitaji uchunguzi wa kina na uchunguzi huu unapokamilika ndipo unapoweza kuletwa Bungeni.

Sasa yapo ambayo tunaona upo umuhimu wa kuyaleta ni pamoja na hayo uliyoyasema, nataka nikuahidi kwamba haya ambayo umeyatamka kwenye maeneo yanayogusa Wizara kadhaa ambazo zinatakiwa kuleta taarifa nitafanya ufuatiliaji, pale ambapo tutakuwa tumekamilisha uchunguzi wetu, nitayaleta kwa utaratibu ambao Bunge utakuwa umetoa maelekezo yake. Ahsante sana.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu nina imani utakubali kwamba usalama wa nchi na mahusiano mema miongoni mwa raia ni tunda la mahusiano mazuri kati ya vyama vya siasa, Serikali na vyombo vyote vya dola.

Mheshimiwa Spika, siku za karibuni kumekuwa kuna mwendelezo wa matukio mengi yanayovunja usalama huo, yanayovunja amani na yanayojenga chuki miongoni mwa vyama vya siasa na kuharibu utengamano wetu wa kitaifa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tukio la kushambuliwa kwa risasi kwa nia ya kuua kwa Mheshimiwa Tundu Anthipas Lissu, Mbunge na Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni limezua hofu kubwa sio tu kwa Taifa ila katika Bara zima la Afrika na Jumuiya ya Kimataifa. Nina hakika taharuki hiyo imeharibu sana sura ya Taifa, heshima tuliyokuwa nayo kama Taifa na hatujaona kama Serikali inachukua hatua zozote kujaribu kufanya jambo hili lisiendelee kuharibu image yetu kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu atakumbuka kwamba hapo nyuma vimetokea vifo vya kisiasa. Alifariki Mwenyekiti wetu wa Mkoa wa Geita, Bunge na Serikali tulilizungumza hapa na Serikali ikasema inafanya uchunguzi, hadi leo hakuna hatua iliyochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, akapotea msaidizi wangu Ben Saanane, nikakuomba Waziri Mkuu na Serikali yako iruhusu uchunguzi wa kimataifa ili kutatua tatizo hili, ukasema vyombo vyetu vya ndani vina uwezo hadi leo hakuna lililopatikana. Tumeomba vilevile kushambuliwa kwa Mheshimiwa Tundu Lissu kuchunguzwe na vyombo vya uchunguzi vya kimataifa vilivyo huru, visivyofungamana na upande wowote, bado Serikali inaonekana ina kigugumizi katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, unatupa kauli gani sisi kama chama, Wabunge na Taifa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nieleze kwamba amani yetu na utulivu ndani ya nchi ni jambo ambalo Watanzania wote lazima tushikamane na tushirikiane katika kulidumisha. Ndilo ambalo linaendelea kutupa heshima duniani kwa sababu Watanzania wote tunashirikiana katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo matukio yanajitokeza, Mheshimiwa Mbowe umezungumzia upande wa siasa lakini pia matukio haya yapo kwa ujumla wake nchini kwenye maeneo kadhaa kwa ngazi ya familia, lakini pia na maeneo mbalimbali ya mikusanyiko, na watu wengine pia. Wapo wenzetu ambao hawana nia njema nchini wanajitokeza katika kutenda matendo hayo.

Mheshimiwa Spika, na hata hili analolisema la Mheshimiwa Tundu Lissu si Mheshimiwa Tundu Lissu pekee ingawa hatupendi mambo kama hayo yatokee, lakini pia tumepoteza Watanzania wengi. Hata mnakumbuka Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji tumepoteza watu wengi. Hata hivyo pia hata siku za karibuni Kamanda wetu wa Jeshi la Ulinzi nchini (JWTZ) naye alipigwa risasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuyazungumze haya kwa ujumla wake na tunapoyazungumza haya kwa ujumla wake, na kwa utamaduni ambao tumeujenga wa nchi hii katika kujilinda wenyewe na kuhakikisha kwamba nchi inaendelea kuwa salama, nataka nikuhakikishie kwamba vyombo vyetu vya dola vinaendelea kufanya uchunguzi wa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na uchunguzi huu hauwezi kuwa wa leo leo ukapata ufumbuzi kwa sababu wanaotenda matendo haya wanatumia mbinu nyingi za kujificha. Kwa hiyo, na sisi lazima tutumie mbinu zetu za kutambua hao waliotenda matendo hayo katika kila eneo ili pia baadaye tuweze kutoa taarifa ya jumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niendelee kukuhakikishia pia kwamba vyombo vya dola haviko kimya, vinaendelea. Nataka nikuhakikishie vilevile kwamba vyombo vyetu vya dola vinao uwezo wa kusimamia usalama ndani ya nchi, ni suala la muda ni wakati gani wanakamilisha taratibu na hatua gani zichukuliwe. Sasa hilo linategemea na waliotenda matukio na namna ambavyo wamejificha na namna ambavyo na sisi tunatumia njia mbalimbali za kuweza kuyapata haya na kuweza kujua na kutoa taarifa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nikusihi na familia zote ambazo zimepata athari na zimeripoti polisi na wameripoti kwa vyombo vya dola na vinaendelea kufanya kazi kwamba, pale ambapo tutakamilisha uchunguzi tutatoa taarifa kwa ngazi ya familia ambazo pia zimepata athari au ndugu au jamaa kupata athari hiyo na kuwaambia hata hatua ambayo sisi tunaichukua pia. Kwa hiyo, nataka niwasihi kwamba jambo hili tuendelee kujenga imani kwa vyombo vyetu vya dola vitakapokamilisha kazi zake vitatoa taarifa.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi. Mheshimiwa Waziri Mkuu ni miaka minne sasa tangu Serikali yenu imeweka zuio kwa vyama vya siasa kufanya wajibu wake kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Nchi. Na tunachozungumza leo Mheshimiwa Waziri Mkuu ni siku 262 zimebaki kufika tarehe 24, 25 Oktoba siku ambayo nchi yetu itafanya uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa busara zako binafsi na ni Serikali ambayo wewe ni kiongozi mwandamizi, mnafikiri ni lini mtaruhusu vyama vya siasa vifanye wajibu wake wa uenezi kujiandaa kwa uchaguzi Mkuu?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili Serikali ina mpango gani wa kuwezesha Taifa kupata Tume Huru ya Uchaguzi ambayo itahakikisha kwamba uchaguzi huu unakuwa huru wa haki na wa halali? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbowe Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza Mheshimiwa anaomba kujua ni lini vyama vya siasa vitaruhusiwa kufanya shughuli zake za kisiasa. Vyama vya siasa havijazuiwa kufanya shughuli zake, ila tumeweka taratibu muhimu unaowezesha vyama kufanya shughuli zake za kisiasa kama ambavyo tumetoa, kumekuwa na uhuru pia wale wote wanasiasa wote ambao waliomba ridhaa kwenye maeneo yao wakapata ridhaa hiyo kuendelea kufanya shughuli na maeneo yao ambayo wamepata ridhaa. Kama vile Madiwani, Wabunge wanaendelea kufanya shughuli zao za siasa kwenye maeneo yao kama ambavyo wao wanapaswa kufanya shughuli hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia amezungumzia lini tunajiandaa kwa ajili ya uchaguzi, ratiba za uchaguzi zitatolewa na ratiba hizi zitaeleza kuanzia lini shughuli za kampeni zitaanza mpaka lini ili vyama viende sasa kama chama kikaeleze sera zake kwenye maeneo yote ili sasa wananchi waweze kupata fursa ya kuendelea kufanya maamuzi ya sera ipi ya chama gani, inafaa kutuletea maendeleo nchini. Kwa hiyo hilo linaendelea na wote mnajua hata kulipokuwa na chaguzi ndogo pale ratiba ilipokuwa inatolewa kila chama kilikuwa kinaendelea kushiriki na huo ndio utaratibu ambao unaifanya hata nchi kuwa imetulia na watu wote kufanya shughuli zao kama kawaida na tutaendelea kufanya hivyo kwa vyama vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuhusu suala la Tume Huru. Jambo hili hata Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu juzi alitoa maelezo hapa, na mimi nataka nirudie tu; kwamba tume hii imeundwa kwa mujibu wa Katiba wa sheria, na kwa mujibu wa Katiba ya nchi kipengele 74 (7), (11), (12) inaeleza kwamba hiki ni chombo huru.

Kimeelezwa pia kwenye Katiba pale kinaundwaje; na chombo hiki hakipaswi kuingiliwa na chombo chochote; iwe Rais wa nchi, iwe chama chochote cha kisiasa au Mamlaka nyingine yoyote ile haipaswai kuiingilia. Kama ni chombo huru kwa mujibu wa Katiba ndiyo Tume huru. Sasa kunaweza kuwa kuna tofauti ya neno huru hili linataka litambulike vipi lakini chombo kipo kinajitegemea kinafanya kazi yake bila kuingiliwa na mtu yoyote, kwa mujibu wa Katiba yetu ya Mwaka 1977. Hayo ndiyo maelezo sahihi na ndiyo ambayo yapo kupitia Katiba na sheria ambazo tumezitunga sisi wenyewe. Ahsante. (Makofi)