Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Dr. Godwin Oloyce Mollel (5 total)

MHE. ABDALLAH H. ULEGA (K.n.y. MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) aliuliza:-
Shamba la Garagua linalomilikiwa na KNCU lililopo katika Wilaya ya Siha, liliamuliwa liuzwe mwaka 2015 ili kulipa mkopo wa shilingi bilioni nne uliochukuliwa na KNCU na baadaye kushindwa kufanya marejesho ya mkopo huo kwa wakati:-
(a) Je, ni kwa nini Serikali isiwawajibishe viongozi wa KNCU waliousababishia ushirika hasara kwa kuchukua mkopo ambao wameshindwa kuulipa?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuyarudisha mashamba ya ushirika yanayotumika kwa maslahi ya wachache au ambayo ushirika umeshindwa kuyaendeleza katika umiliki wa Halmashauri za Wilaya husika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Siha, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Chama Kikuu cha Ushirika cha KNCU Limited kilishindwa kulipa deni la shilingi bilioni 3.4 kutoka CRDB lililokopwa misimu ya 2008/2009 hadi 2010/2011. Ili kubaini sababu za kushindwa kurejesha mkopo, Wizara iliagiza Mrajisi wa Vyama vya Ushirika nchini kufanya ukaguzi na uchunguzi ili kujua kiini cha KNCU kushindwa kulipa deni hilo. Ukaguzi na uchunguzi huo ulibaini hasara ya sh. 3,946,755,736 uliosababishwa na mdodoro wa uchumi na ubadhirifu na uongozi mbovu wa KNCU. Hivyo, Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika ilisimamisha Bodi iliyokuwa madarakani ambayo ilisababisha hasara na kuweka Bodi mpya kama hatua ya awali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine, Wizara kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika imeanza kuandaa taratibu za kuwachukulia hatua wahusika kwa mujibu wa kifungu cha 15(33) cha Sheria ya Ushirika Na. 6 ya 2013. Aidha, katika kunusuru uuzaji wa mali za KNCU, Mkutano Mkuu wa KNCU uliokaa tarehe 22 Oktoba, 2014 uliazimia kuuzwa kwa shamba la Garagua ili kulipa deni hilo la CRDB na madeni mengine.
(b) Kwa mujibu wa takwimu ambazo Tume ya Maendeleo ya Ushirika inazo, yapo mashamba 96 ya Vyama vya Ushirika nchi nzima yakiwemo 41 Mkoa wa Kilimajaro. Kati ya hayo, mashamba saba yapo Wilaya ya Siha ambapo matatu yanamilikiwa na KNCU na mengine manne yanamilikiwa na Vyama vya Msingi. Mengi ya mashamba haya yamekuwa yakitumika kwa kilimo, ufugaji na ujenzi wa nyumba za makazi ya wanachama na kukodishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kushirikiana na MKURABITA, TAMISEMI na Vyama Vikuu vya Ushirika nchini inakamilisha maandalizi ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi. Mpango huu unatarajiwa kuwasilishwa kwenye kikao kazi kinachofanyika Dodoma, Ukumbi wa Hazina tarehe 27, yaani leo na 28 Juni, 2016. Kikao hicho kitajumuisha Vyama Vikuu vyote vya Ushirika nchini na kukubaliana mkakati wa kuyaendeleza mashamba hayo kwa manufaa ya wanachama na halmashauri kwa ujumla.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL aliuliza:-
Mafunzo na mazoezi ya kijeshi yanayofanywa na Chuo cha Polisi (CCP) katika eneo la Kata ya Donyomorwa katika Wilaya ya Siha yamesababisha maafa makubwa kwa wananchi ikiwa ni pamoja na wananchi kuuawa kwa risasi na mabomu yanayotumika katika mazoezi hayo.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamisha mafunzo hayo kutoka kwenye maeneo ya makazi ili kuepusha maafa yanayowapata wananchi wa maeneo hayo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Siha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina mpango wa kuhamisha mafunzo ya kijeshi katika eneo la Donyomorwa. Awali mafunzo hayo yalikuwa yakifanyika katika eneo la Kilelepori ambalo lilivamiwa na wananchi kwa kujenga nyumba na kufanya shughuli za kilimo ambapo Serikali iliamua kuhamisha mafunzo ya kijeshi katika eneo hili nililolitaja sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuepusha madhara yanayoweza kuwapata wananchi, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa jamii ya Kimasai kuacha kuchunga mifugo katika eneo hilo, kukata kuni na kuokota kitu chochote wasichokijua katika eneo hilo. Aidha, kabla ya Polisi kuanza mazoezi ya kijeshi huchukua tahadhari kama kutoa taarifa kwa Vijiji, Wilaya na Mkoa ikiwa ni pamoja na kuweka alama za tahadhari kuzunguka eneo lote kwa kuweka bendera nyekundu na kuwaweka askari katika vipenyo vya kuingia katika eneo hilo.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL aliuliza:-
Ushirika katika Wilaya ya Siha umekumbwa na matukio ya ufisadi yakiwemo upotevu wa zaidi ya shilingi milioni 840 katika Ushirika wa Siha Kiyeyu, upotevu wa shilingi milioni 337 ya SACCOS ya Sanya Juu pamoja na matumizi mabaya ya ardhi, licha ya uchunguzi mzuri uliofanywa na TAKUKURU Mkoa:-
Je, ni kwa nini uchunguzi huo unaingiliwa na maslahi binafsi ya watu wachache na kusababisha matukio yanayodhalilisha Serikali?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kujibu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Jimbo la Siha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kifungu cha 5 (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya Mwaka 2007, TAKURURU imepewa mamlaka kuwa chombo huru cha kuzuia na kupambana na rushwa nchini; na inatekeleza majukumu yake muhimu kama yalivyofafanuliwa katika Kifungu cha (7) cha sheria hiyo ya kuzuia na kupambana na rushwa. Kutokana na mantiki hiyo ya kisheria, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa namna yoyote ile, Taasisi ya TAKUKURU haiwezi kuingiliwa na mtu yeyote.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba TAKUKURU ilipokea tuhuma za udanganyifu wa matumizi ya fedha za umma kutoka katika vyanzo vyake mbalimbali zilizokihusu Chama cha Ushirika cha Siha Kiyeyu na Sanya Juu SACCOS. Kutokana na tuhuma hizo, uchunguzi uliofanywa na TAKUKURU ulithibitisha pasipo shaka kwamba viongozi wa Chama cha Ushirika Siha Kiyeyu bila ridhaa ya wanachama wake, waligawa mashamba kwa watu wasio wanachama wapatao 13, shamba lenye ekari 16 ambazo zililimwa kati ya miaka miwili na mitano bila ya kulipiwa gharama yoyote. Kitendo hiki kiliukosesha ushirika Siha Kiyeyu mapato ya kiasi cha sh. 1,600,000/=.
Mheshimiwa Spika, uchunguzi pia ulithibitisha pasipo shaka kwamba uongozi wa Chama cha Msingi cha Ushirika cha Siha Kiyeyu ulitoa maelezo ya uongo kwa Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa William Olenasha kwa kumpatia stakabadhi za uongo juu ya matumizi ya sh.500,000/= za ushirika kwa ajili ya semina. Baada ya uchunguzi kukamilika uongozi huo ulikiri kutenda kosa hilo mbele ya wachunguzi.
Mheshimiwa Spika, tuhuma kuhusu ufisadi wa sh.337,000/= unaoihusu SACCOS ya Sanya Juu ni tuhuma mpya. Tuhuma za Sanya Juu SACCOS zilihusu kiasi cha sh.160,100,406, na tuhuma hizi zilichunguzwa na Jeshi la Polisi na kesi Na. CC 15/2016 imeshafunguliwa na ipo katika Mahakama ya Wilaya ya Siha.
Mheshimiwa Spika, tuhuma za upotevu wa shilingi milioni 840 unaokihusu Chama cha Ushirika cha Kiyeyu ni malalamiko ya wanachama juu ya tozo anazolipa mwekezaji katika shamba la maparachichi ambapo anadaiwa kulipa kiasi cha shilingi milioni 60 kwa mwaka. Tuhuma hizi ni mpya na Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Kilimanjaro imezipokea kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Uchunguzi utakapokamilika, taarifa itatolewa.
MHE. JULIUS K. LAIZER (K.n.y MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) aliuliza:-
Wilaya ya Siha ina changamoto ya upungufu wa ardhi jambo ambalo limesababisha wananchi kushindwa kuendesha shughuli zao za kiuchumi kwa ufanisi na pia kuendeleza makazi yao katika maeneo hatarish.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwagawia wananchi mashamba yaliyoko chini ya Hazina kama vile mashamba ya Foster, Journey’s End na Harlington ili wananchi wayatumie kwa kilimo ikizingatiwa kuwa wananchi Kata ya Nchimeta Ngarenairobi wanaishi kwenye maporomoko hatarishi hasa wakati wa mvua na majanga ya moto?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga ardhi
kwa ajili ya ufugaji kwa wananchi wa Siha ambao kwa sasa hawana maeneo ya malisho kwa mifugo yao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Siha, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, mwaka 2007 Serikali ilitoa maelekezo ya kusitisha uuzaji wa mashamba ambayo yalikuwa hayajabinafsishwa yakiwemo mashamba ya Forester, Journey’s End, Harlington na Kanamodo yaliyopo NAFCO, West Kilimanjaro. Serikali ilisitisha zoezi la uuzaji wa mashamba hayo baada ya wananchi wa Siha pamoja na Uongozi wa Wilaya na Mkoa kupinga zoezi la ubinafsishaji wa mashamba na kupendekeza mashamba hayo yagawiwe kwa wananchi. Serikali ilikubaliana na maoni ya wananchi na hivyo kumtafuta Mtaalam Mwelekezi kufanya utafiti na matumizi bora ya mashamba hayo.
Mheshimiwa Spika, tathmini ilifanyika na mapendekezo yalikuwa kama ifuatavyo:-
(i) Kuyagawa mashamba hayo katika mashamba madogo madogo kwa ajili ya shughuli za kilimo cha mazao na ufugaji kwa wakulima wadogo na wa kati na kisha kuyauza kwa njia ya zabuni; na
(ii) Baadhi ya maeneo kukabidhiwa kwa Halmashauri
ya Wilaya ya Siha kwa shughuli za maendeleo ikiwemo makazi, shule, vyuo, hospitali na magereza.
Mheshimiwa Spika, kwa kutilia maanani mapendekezo ya mtaalam mwelekezi, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ilielekezwa kuandaa Waraka wa Baraza la Mawaziri wenye mapendekezo ya namna bora ya matumizi ya mashamba hayo. Waraka huo ulishawasilishwa na kufikia ngazi ya Makatibu Wakuu na kutolewa maoni kwa ajili ya marekebisho.
Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilisha marekebisho, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi itauwasilisha waraka huo kwenye Baraza la Mawaziri. Baada ya kujiridhisha na mapendekezo na ushauri, Serikali itatoa uamuzi kuhusu matumizi ya mashamba husika.
(c) Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa maelekezo kwa Halmashauri zote nchini kukamilisha mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Waheshimiwa Wabunge, sisi ni sehemu ya Baraza la Madiwani katika maeneo yetu, hivyo tunapaswa kusimamia maelekezo ya Serikali ili kuhakikisha kuwa wafugaji na wakulima wanatengewa maeneo yao. Tuhakikishe kila kundi linatengewa maeneo kwa ajili ya shughuli zao za kiuchumi. Hapo tutakuwa tumeandaa msingi bora wa maendeleo ya kiuchumi kwa watu wetu.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL aliuliza:-

Aliyekuwa Naibu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Olenasha alitembelea Wilaya ya Siha kufuatilia ubadhirifu kwenye Shamba la Ganrangua na SACCOS ya Sanya Juu wa shilingi milioni 337 na Siha Kiyeyu shilingi milioni 840 ambapo aliiagiza TAKUKURU kuchunguza ubadhirifu huo:-

(a) Je, Serikali iko tayari kufanya upembuzi na kutambua mashamba ya umma, yasiyotumika vizuri na kurejesha kwa wananchi kwa kutumia vijiji na ushirika wao kama wazo la kwanza la Baba wa Taifa J. K. Nyerere, mfano wa baadhi ya mashamba hayo ni Kafoi Farm (Mifugo), Leoni(Ushirika-Mfilisi), Msingi (Ushirika-Mfilisi), Pirita (Ushirika- Mfilisi), Pongo (Ushirika-Mfilisi) na mengine mengi?

(b) Pamoja na juhudi nzuri zilizofanywa na Waziri Mkuu kuhusu ubadhirifu KNCU, je, Serikali ina taarifa kuwa ubadhirifu kwenye mali za KNCU na Vyama vya Ushirika ni mkubwa na unaendelea kulindwa na wahusika hawagusiki na bei ya zao la kahawa linaendelea kuathirika?

(c) Je, Serikali inaweza kuwaeleza nini wananchi wa Siha kuhusu Shamba la Gararagua lililouzwa na KNCU mwaka 2014 na makabidhiano kufanyika mwaka 2016, likitoka mkononi mwa Ocean Link lakini Kampuni hii mpya imepata EPZ Exemption mwaka 2012 na je, Serikali haioni kuna harufu ya ufisadi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Jimbo la Siha, lenye sehemu (a),(b) na (c), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upembuzi na utambuzi wa mashamba umekuwa ukifanywa na Serikali kila inapohitajika ili kufanya maamuzi sahihi ya matumizi ya mashamba. Mashamba ya Leoni, Msingi, Pirita na Pongo yanamilikiwa na Vyama vya Ushirika isipokuwa Shamba la Kafoi ambalo linamilikiwa na mtu binafsi. Mashamba haya yalikuwa na migogoro kwa muda mrefu kati ya vyama na wawekezaji ambao kwa sasa migogoro hiyo imekwishatatuliwa. Aidha, Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika inasimamia kwa karibu vyama husika ili kupata wawekezaji wapya kwa maendeleo ya wanachama wa Vyama vya Ushirika na wananchi wa Vijiji vya Wilaya ya Siha.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imechukua hatua kwa viongozi na watendaji waliobainika kujihusisha na ubadhirifu wa mali za KNCU kwa kuwafikisha Mahakamani kwa kesi ya uhujumu uchumi. Aidha, Serikali kwa kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika kutekeleza jukumu lake la ukaguzi wa mara kwa mara kwa Vyama vya Ushirika, itaendelea kufanya ukaguzi kwa Vyama vya Ushirika, ikiwemo KNCU na pale itakapobainika kuwa kuna ubadhirifu wa mali za vyama, Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaohusika bila kujali nyadhifa au uwezo wa aina yoyote walionao.

Mheshimiwa Spika, Shamba la Gararagua limeuzwa na KNCU mwaka 2014 kwa kuzingatia taratibu za manunuzi. Aidha, msamaha wa kodi yaani exemption uliotolewa kwa mwekezaji huyo mwaka 2012 unahusiana na uwekezaji wa Shamba la Kifufu na siyo Gararagua.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tuhuma za ufisadi, Wizara itafuatilia suala hilo na itakapobainika kuna viashiria hivyo, Serikali itachukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.